Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kuunga mkono hoja. Pili, nianze kwa kukushukuru sana wewe na pia nimshukuru sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Shukrani zangu zina msingi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipata heshima ya kukusimamia Masters yako na uliandikia kuhusu The Rights to Clean and Health Environment na case study yako ilikuwa ni Geita Gold Mine. Ingawa nilikusimamia lakini nilijifunza na sikujua hayo ni maandalizi ya baadaye ndani ya utumishi wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nimshukuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye na yeye nilimsimamia PhD yake katika somo hili hili alilolizungumza leo na yeye kwake nimejifunza sana. Sikujua kwamba nilikuwa naandaliwa kuja kufanya kazi ambayo itahusiana na hawa wanafunzi wangu wawili ambao pia ni walimu wangu wakati huo, yaani Naibu Spika na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ni heshima kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, nimshukuru sana na mimi Mwalimu wangu aliyenisimamia PhD yangu Ujerumani, chuo ambacho sasa kinafikisha miaka 70 na yeye amestaafu. Kwa sababu miaka ile ya mwisho wa 80 na mwanzo wa 90 wakati tunayazungumzia haya aliyoyaeleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa nchi za Ulaya yalikuwa ni mapinduzi makubwa. Sikujua kwamba baadaye nitapata fursa ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kunipa fursa ya kuitumikia nchi hii na kunipa jukumu la kuisaidia nchi hii kutunga sheria hizi za madini na mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, falsafa na muktadha wa usimamizi wa madini katika nchi zetu umebadilika. Napozungumza falsafa narudi kwenye Kitabu cha Ibrahim Hussein cha Mashetani, yule shetani mmoja aliyekuwa daima anasema weltanschauung, weltanschauung. Weltanschauung maana yake ni muono mpya wa mambo ambayo yalikuwa dhahiri lakini watu walikuwa hawaoni yakiwa dhahiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unyonyaji wa madini yetu na mataifa ya nje lilikuwa ni jambo dhahiri lakini hatukuliona kuwa ni dhahiri na likapambwa, likarembeshwa likafanya kuonekana ni jambo la kawaida na tukashindwa kutofautisha kati ya uwekezaji (investment) na unyonyaji (exploitation). Kwa hiyo, kwa muda wote huu sheria zetu za madini zilijikita katika unyonyaji (exploitation) na hatukuwa tumeweka mazingira mazuri ya uwekezaji (investment) kwa faida ya nchi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hatua tulizozichukua ni hatua za kimapinduzi na ni lazima zipingwe kwa nguvu zote na wale wote waliokuwa wanafaidika na hali hiyo. Kwa hiyo, ni jukumu letu kusimama kidete pamoja na Rais wetu kuhakikisha kwamba hii weltanschauung (msimamo) mpya tunausimamia kwa nguvu zetu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana mingoni mwa mambo makubwa ambayo yamefanywa na sheria hii ni kuondoa kabisa Mining Development Agreements, zilizoingiwa ndizo za mwisho. Kuanzia sheria hii ilipopitishwa, hakuna tena MDA ni Special Mining License, Mining License na Primary Mining License. Kwa sababu ya matatizo ya utendaji ndani ya Wizara na Kamisheni sasa Special Mining License na Mining License zitatolewa kwa kibali cha Baraza la Mawaziri. SML ni Baraza la Mawaziri ili Serikali nzima ishiriki katika kuhakikisha kwamba leseni za madini za wachimbaji wakubwa zinatolewa kwa manufaa na maslahi ya nchi yetu, hakuna tena MDA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunahangaika na MDA zilizokuwa zimeingiwa lakini hakutakuwa na mpya ili tuondokane na kuwa na matabaka mawili ya wachimbaji wanaochimba kwa leseni na wanaochimba kwa mikataba maalum, wote sasa watachimba kwa masharti ya leseni na asiyetaka hivyo asije. Madini haya babu wa babu zetu, babu zetu, baba zetu na sisi tumeyakuta hayajaoza, asiyetaka kuja kuchimba madini haya kwa masharti haya ayaache na sisi tutakufa, tutazikwa watakuja watoto, wajukuu na vitukuu wetu watavikuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusema madini ni utajiri unaokwisha na ni muhali kuyatumia kwa matumizi ya kawaida. Ni lazima yatumike katika uwekezaji wa kukuza ustawi wa watu na maendeleo ya nchi katika miundombinu na viwanda na uwekezaji wa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yoyote inayochimba madini for recurrent expenditure imefilisika. Madini ni lazima yaende katika strategic investment; standard gauge railway, Stiegler’s Gorge, viwanda na miundombinu. Maana yake tuvune madini kwa kiasi, tusiyavune madini kwa pupa kama vile mwisho wa dunia ni sisi, tutakufa tutaiacha nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuvune madini kwa kiasi ili vizazi vijavyo navyo viyakute madini na yale tutakayokuwa tumeyachimba wakute faida yake katika sekta nyingine za uchumi; miundombinu, vyuo vikuu, viwanda. Hivyo ndivyo ilivyofanya nchi ya Nigeria na ndiyo hilo Naibu Spika ulilizungumzia katika Taslifu yako ya Masters, intergeneration equity. Sisi kwa lugha ya zamani ni mawakili wa mali za Mungu siyo kwa matumizi yetu sisi tu lakini kwa vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naonya hii shauku/hamu/pupa ya kutaka tuyachimbe madini yote; tuyabakize mengine kwa viazi vijavyo. Bara la Afrika tumekuwa tunasukumwa na nchi za nje kutaka tuchimbe madini yetu kwa namna hiyo. Ndiyo maana baada ya hatua hii iliyochukuliwa, nashukuru sana nchi nyingine za Afrika zimefuata na nchi ya mwisho ambayo nilitegemea ingefuata mfano wa Tanzania ni Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Zambia wamefanya hivyo na nchi nyingine ili tuyatunze haya madini ya Afrika kwa vizazi vijavyo kama ambavyo Norway wao mafuta wanayoyachimba wanaweka akiba kwa ajili ya vizazi vijavyo na kuna fedha ambayo imewekwa itatumika miaka 50 baada ya tone la mwisho la mafuta na gesi ya mwisho kwisha. Kwa hiyo, unaona wenzetu wanavyofikiria na sisi pia ndiyo malengo ya sheria hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mabadiliko haya ya kisheria, Mheshimiwa Rais ametusaidia sana, moja ni la makinikia. Makinikia yalisemwa si mali ni mchanga hauna maana lakini sote tumeona mara baaada ya makinikia kuzuiwa kwenda nje ndiyo tumejua kwamba makinikia ni mali, ni rasilimali. Ndiyo maana ndani ya mabadiliko ya Sheria ya Madini ya mwaka 2017 imetamka wazi kuwa sasa makinikia nayo ni mali inayouzwa kama mali inayojitegemea, si kama sehemu ya yale madini yaliyokuwa yamepimwa. Kwa hiyo, limetusaidia na ndiyo maana tangu sheria hii imetungwa hakuna makinikia ambayo yameshatoka nje ya nchi ili uwekwe utaratibu wa kuyaongezea thamani makinikia kama bidhaa inayojitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo hatukulijua ndani ya makinikia kuna aina ya madini ingawa kiasi chake ni kidogo lakini yana thamani kubwa sana yanaitwa rare-earth, ya thamani kubwa sana. Kwa hiyo, utaratibu mpya umekwishafanyika na kanuni zimekwishatungwa na Mheshimiwa Waziri zitakazosimamia suala hilo la makinikia na itakuwa ni marufuku kuyasafirisha makinikia nje ya nchi kinyume na masharti yaliyowekwa na Sheria ya Madini na Kanuni zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya mambo ambayo pia yamezungumzwa na kuulizwa sana hapa ni kuhusu kishika uchumba cha majadiliano kati ya Barrick na Tanzania. Kwanza nichukue fursa hii tena kumshukuru Mwenyezi Mungu na pili nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani kubwa sana aliyotupa sisi kusimamia majadiliano hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sakata hilo lilipoanza tulitishwa, tuliambiwa tutafilisiwa, hatutafika popote na hiyo ndiyo ilikuwa sababu kwa kiasi kikubwa ya kuwaficha wajumbe wengine kwa sababu bahati mbaya nchi yetu tumeacha kujadili masuala, tunajadili watu. Watu wangejua mmoja wa wajumbe hao ni Chacha, basi huyo Chacha angechambuliwa mpaka angechacha kama chakula kilichokaa siku nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mazungumzo yale yaliyokamilika tarehe 19 Oktoba, 2017 yalikuwa ya mafanikio. Mafanikio mimi kama mmoja wa watu walioshiriki, siyo kile kilichopatikana lakini kile ambacho kimetuwezesha sasa kuangalia Tanzania ya kesho katika matumizi yake ya madini. Hii ni kwa sababu tumerithi mikataba ambayo iliyokuwa ina matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yale makubaliano yalikuwa makubaliano ya msingi na baada ya hapo tumeingia katika majadiliano ya kina ambayo napenda kusema kwamba yanaendelea vizuri kati ya timu ya Serikali na Barrick na majadiliano hayo yanakaribia kufikia hatma yake. Kwa mujibu wa ratiba ambayo tulikuwa tumepeana, mwisho wa mwezi Juni au katikati ya Julai tutakuwa tumefikia katika hatua za mwisho na ukamilishaji wake ni pamoja na utaratibu wa ulipwaji wa malipo hayo ya Dola milioni 300. Kwa hiyo, tunaendelea na Inshallah, ndiyo maana ya neno Inshallah, maana Inshallah ni mapenzi ya Mungu (Allah) siyo hiyari yako, Inshallah, Inshallah mazungumzo hayo yatazaa matunda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba shughuli hiyo haikuishia tu na Barrick, tunafanya mazungumzo na kampuni nyingine. Tumekwishamaliza mazungumzo na Kampuni ya Tanzanite One Mining Limited, mazungumzo ambayo yalifanikiwa na kusainiwa makubaliano tarehe 15 Aprili, 2018. Wao wamekiri makosa waliyoyafanya, watalipa kodi na tozo zote na pamoja na hiyo watatoa fidia kwa Serikali; na tayari installment ya kwanza ya fidia hiyo imeshalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunaishi dunia ambayo tumejifunza, utakapotaja mambo kama hayo wale wasiotutakia mema ambao wanafungua kesi kesho na keshokutwa, watajua mna kiasi gani maana yake nyumba yenye fedha/mali ndiyo wezi huinyemelea. Ndani ya Serikali na kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali atajua fedha hizo zilipoingia na zilipo kwa sababu haziingii kama maduhuli ya Wizara ya Madini, zinaingia kama fidia kwa Taifa na zina utaratibu wake na zinasimamiwa na Katibu Mkuu Kiongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nchi tumejifunza hata hiyo fidia hatutaitamka katika kadamnasi lakini ndani ya Serikali na wale wanaoruhusiwa kujua watajua ni kiasi gani Tanzanite One Mining Limited wamelipa. Maana yake tumejifunza sasa hivi kesi zimeongezeka kwa sababu wanajua tuna hela, kwa hiyo ni upuuzi pia kusema kila kitu. Unapowaambia watu una pesa unaita watu kuja kukuibia lakini fedha ipo, utaratibu upo, Paymaster General na Auditor General yupo na nashukuru sana Tanzanite One Mining Limited kwa kutekeleza ya kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeanza pia mazungumzo na Ashanti Gold na tutaendelea nayo tena Julai, tumekwishakutana nao mara moja. Tutafanya majadiliano na kampuni nyingine za tanzanite, kampuni kama 10 zinazovuna tanzanite. Tutafanya mazungumzo na kampuni zote, Kampuni ya Williamson Diamond Limited ambayo karibu tutaanza nao mazungumzo lakini pia Al - Hillary.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni mlolongo wa mazungumzo na kila yatakapokwenda Taifa litakuwa linaarifiwa, lakini kwa muktadha na hali ya leo kiasi cha fedha kitaingizwa Hazina na hatutapenda kukitangaza sana na watu watafahamu kwa njia nyingine ili tuepukane na hali ambayo tumejifunza kwamba baada ya watu kujua tuna fedha, tunajenga standard gauge railway, tumenunua ndege saba sasa yanakuja madeni mengine ya miaka ya 70. Mtu alikuwa na deni toka mwaka 1978 leo ndiyo analikumbuka, nje huko na ukilisoma unajiuliza tangu mwaka 1978 huyu mtu hizi fedha mbona alikuwa hadai, ni kwa sababu sasa wamejua kuna kitu. Kwa hiyo, nawaomba Watanzania watuelewe, waielewe Serikali yao na waivumilie inapopambana na hali hii ya unyonyaji mkubwa na hatua ambazo imezichukua ili kuyarekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nimpongeze sana Waziri wa Madini na Naibu Mawaziri wa Madini. Naomba tena kurudia kuunga mkono hoja, niliogopa nisije nikapigiwa kengele kabla sijaunga mkono hoja mwanzoni, ahsante.