Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, ili niweze kuchangia hoja hii ya mipango. Kwanza kabisa nianze na sekta ya umeme; niishukuru sana Serikali imejitahidi kuhakikisha kwamba vijiji vingi vinakuwa na huduma ya umeme. Kwa Jimbo la Mpwapwa ni vijiji sita tu ambavyo bado havijapata huduma ya umeme kwa hiyo, nishukuru na niipongeze sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya umeme ni maendeleo ya nchi na uchumi wa nchi kwa sababu, kijiji kikipata umeme wataanzisha viwanda vidogovidogo vya kukamua mbegu za mafuta kwa mfano alizeti, ufuta, karanga na Serikali itapata mapato pale. Kwa hiyo, naiomba Serikali, namwomba sana Mheshimiwa Waziri na ameshafika Mpwapwa kutembelea kuona hii hali ya huduma za umeme, vile vijiji ambavyo bado havijapata umeme Kazania, Kiyegeya, Chimaligo, Mkanana, Kiboliani, Nana, Namba 30 Mafuto pamoja na Majami, naomba sana Mheshimiwa Waziri ajitahidi nao wapate umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni sekta ya ujenzi. Mawasiliano ni muhimu sana katika nchi yoyote duniani, bila mawasiliano nchi hiyo itakuwa haina maendeleo. Barabara za lami zinatengenezwa, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais amesimamia hiyo kazi hasa Dar-es-Salaam ambako kuna msongamano mkubwa sana wa wananchi, lakini haya mabasi yanayokwenda kasi yamepunguza msongamano, lakini hata fly overs ambazo zinajengwa zimesaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikumbushe suala la ujenzi wa barabara. Pamoja na kwamba, Serikali inajitahidi kujenga barabara za Kitaifa na mkoa, lakini hata hizi za wilaya kwa mfano, barabara ya kutoka Mbande – Kongwa – Mpwapwa, hili suala nimeshalizungumza muda mrefu sana hata Mheshimiwa Waziri Mkuu wiki mbili zilizopita alikuwa Mpwapwa tumeshamwambia ni ahadi ya Marais karibu wanne wote wanaahidi kwamba, tutatengeneza hii barabara kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni muhimu sana kwa maendeleo ya Wilaya ya Mpwapwa na uchumi wa Mpwapwa, kwa hiyo, naiomba sana Serikali kwa mwaka huu wameitengea fedha ni kidogo sana, milioni 500 ni sawasawa na kilometa moja tu. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, Waziri wa Mipango wakati anasoma alikuja Wilaya ya Mpwapwa kufanya mazoezi na barabara ile alipita, anaifahamu vizuri sana, hebu wanisaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara za vijijini ni muhimu. Tusiseme kwamba barabara za lami tu, ndio barabara za lami ni muhimu, lakini vijijini ndiko wanakoishi wakulima na watu wa mijini wengi hawana mashamba, hawalimi, wanategemea chakula kutoka vijijini, sasa magari yasipopata barabara nzuri za kupita watasafirishaje haya mazao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA ni kweli imeundwa naishukuru Serikali, lakini iongezewe bajeti. Naomba lile fungu lile la mafuta, Mfuko wa Road Fund, basi angalau tugawane TANROADS wapate 60% na TARURA wapate 40% waweze kufanya matengenezo ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zetu ni mbaya sana. Waziri wa TAMISEMI ameshafika maeneo ya Mima, Barabara ya Mima ni mbaya haipitiki, sasa na mvua zinaanza, Barabara za Mkanana. Naishukuru sana Serikali imetenga milioni 48 na kwa upande wa barabara ya Mima imetengewa zaidi ya milioni 60 na tayari Wakandarasi wameshasaini mikataba kwa hiyo, hivi karibuni wataanza kutengeneza. Kwa hiyo, pamoja na barabara za Kitaifa, barabara za Mikoa, lakini vilevile Serikali izingatie barabara za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni sekta ya maji, sekta ya maji ni muhimu sana, maji ni uhai, maji ndio uchumi wetu, maji ndio maendeleo na maji ndio kila kitu. Kwa hiyo, naiomba Serikali pamoja na juhudi kwamba, visima vya maji vimechimbwa karibu vijiji vingi sana; kwa mfano mimi katika jimbo langu visima vimechimbwa vingi, lakini bado wananchi wana tatizo la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwasaidie akinamama kusafiri mwenda mrefu, ukiwa na ndoo, ukiwa na sijui kitu gani unakwenda kutafuta maji kilometa 10 mpaka 15. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali suala la huduma ya maji ni muhimu sana. Naishauri Serikali kila kijiji kiwe na kisima cha maji ili kuwapunguzia hawa akinamama matatizo ya kusafiri mwendo mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta nyingine ni sekta ya afya, ni kweli Serikali imejitahidi sana maana afya, ukisema Wizara ya Afya ni hospitali, vituo vya afya na zahanati na zahanati, hospitali, vituo vya afya si majengo tu isipokuwa ni dawa, lazima majengo hayo yawe na dawa za kutosha na yawe na watumishi wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi za Serikali kutenga fedha za kutosha karibu bilioni 269 kwa ajili ya kununua dawa, lakini bado tatizo hili ni kubwa katika hospitali zetu, watumishi ni wachache; utakuta zahanati wanaohudumia zaidi ni wale medical attendant, hatusemi kwamba, hawafanyi kazi nzuri, medical attendant ndio wanafanya kazi nzuri, ndio wanatoa dawa, wanachoma sindano na hata kuzalisha akinamama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali ilikuwa na mpango wa kuanzisha vyuo vingi kwa ajili ya ku-train au kufundisha hawa Clinical Officers au Clinical Assistants, lakini mpaka sasa bado watumishi hao ni wachache sana. Naomba vyuo vile ambavyo Serikali, Wizara ya Afya iliahidi basi vifunguliwe kwa ajili ya kufundisha Clinical Officers pamoja na Clinical Assistants ili waweze kupelekwa kwenye zahanati zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na haya machache, lakini nakushukuru sana. Naiomba Serikali ikumbuke barabara za Mpwapwa, Kongwa, pamoja na Mbande pamoja na Daraja la Godegode ambacho ni kiungo kikubwa cha Jimbo la Mpwapwa na Jimbo la Kibakwe. Hivi sasa wananchi wanazunguka kutoka Kata za Mbuga kuja Kata ya Lumuma, Kata ya Kitatu Pwaga wanazungukia Kibakwe ambayo ni zaidi ya kilometa 100 na nauli ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naunga mkono kwa asilimia mia.