Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ili nami niweze kuchangia katika mpango huu. Nianze kwa kuipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuendelea kupeleka mbele maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuelekeza pongezi zangu za dhati katika maeneo kadhaa ambayo ni dhihirisho la uhakika kinyume na hoja walizotoa wenzetu wa Kambi ya Upinzani kwamba maendeleo ya nchi yetu yanarudi nyuma. Napingana nao kwa sababu hata ukiangalia katika upande wa ukuaji wa uchumi nchi yetu iko katika mstari wa mbele inaongoza katika Ukanda wa Afrika Mashariki kwa kuwa na ukuaji wa asilimia 7.1 mwaka 2017 na mwaka huu asilimia 7.2. Inaonekana kwamba uchumi wetu unakua na hakuna sababu ya kutilia mashaka hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuipongeza Serikali yetu kwa sababu nimeangalia katika baadhi ya mambo yanayotekelezwa nikaona kwamba kuna mapinduzi makubwa katika sekta ya madini. Mabadiliko makubwa yamefanyika katika sera na sheria na mapato yameongezeka, sawasawa na Ofisi ya Msajili wa Hazina, Wizara ya Ardhi na hata Uhamiaji. Nimesoma katika mpango, nami napenda kupongeza hilo na kuishauri Serikali kwamba tuendelee katika kutumia hii teknolojia ya kielektroniki kwani ndiyo imekuwa chanzo cha makusanyo ya Serikali kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningetamani kuona hili likichukuliwa kama kipaumbele cha kwanza na Wizara yetu ya Maliasili na Utalii kwa sababu kuna tozo nyingi ambazo zimetawanyika na zinawakera wateja wetu ambao ni watalii. Natamani kuona kitu ambacho napendekeza kiitwe One Stop Payment Centre ambapo mtalii kwa kutumia mifumo ya mitandao ambayo itaanzishwa anaweza aka- book parks anazotaka kwenda akiwa kwao, akalipia kwa credit card yake fees zinazohusika, akalipia hata visa, akifika airport anaonesha tu kwamba ameshalipia na anaongozwa mpaka kwenye parks zetu akatalii kwa raha zake na kuondoka bila kubugudhiwa. Tukifanya hivyo, naamini sekta ya utalii itaongeza mapato kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuipongeza Serikali katika sekta ya elimu. Ukiangalia sekta hii sasa hivi kuna sera ya elimu msingi bila malipo ambayo imeongeza idadi ya watoto wanaosoma. Pia napenda kuipongeza Wizara kwa sababu wameonesha jitihada katika kuchapisha vitabu vya kiada na rejea hata katika ngazi ya chini kuanzia elimu ya awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri kwamba kwa sababu tuna azma kubwa ya kufundisha wataalam wa fani mbalimbali katika nchi yetu, hatutaweza kuwa na wataalam wabobevu na wenye msingi imara tusipowekeza katika elimu ya awali kwa kuhakikisha kwamba hizi shule zinazoitwa shule shikizi ambazo jamii ndiyo inawatafuta walimu, tena ambao hawajasomea, naiomba Serikali iweke katika huu mpango wa mwaka huu unaokuja mkakati kabambe wa kuhakikisha kwamba shule shikizi zinasimamiwa na Serikali ama kwa kuwapelekea walimu au kwa kuhamasisha jamii waaajiri walimu ambao wamesomea jinsi ya kutoa elimu ya awali. Ni katika kutoa elimu bora katika ngazi ya awali ndiyo tunapata watoto ambao wameiva kwenda elimu ya msingi, sekondari, vyuo na kuwapata wataalam katika fani mbalimbali zinazohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilipokuwa napitia hii taarifa ya Kamati wameelezea baadhi ya miradi mikubwa ambayo ingeiletea faida Serikali yetu lakini inaonekana haijawekwa katika mpango wa mwaka 2019/2020. Wametaja mradi mmoja unaoitwa Mradi wa Magadisoda wa Bonde la Engaruka, nafikiri wamekosea na wakasema upo katika Ziwa Manyara, ni ukurasa wa 22 lakini Bonde la Engaruka haliko katika Ziwa Manyara liko katika Wilaya ya Monduli na Bonde hilo lina ziwa kwa lugha yetu ya Kimasai linaitwa Orboloti Langaruka, ni eneo la mpakani mwa Longido na Monduli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba katika kuangalia kwa kina manufaa ya mradi huu kwa jamii zinazozunguka eneo hilo, watakapokuwa wanafanya usanifu na naamini umeshafanyika, ili kuepusha migogoro wabainishe uhalisia wa maeneo yaliyopo katika Wilaya ya Monduli maana asilimia kubwa ya ziwa liko katika Wilaya ya Monduli lakini kuna maeneo pia ya bonde hilo ambayo yanaangukia katika Wilaya ya Longido. Napenda kutoa ushauri huo ili kuepusha migogoro ambayo inaweza ikazuka baadaye wananchi watakapokuwa wanadai manufaa yatakayotokana na mradi huo wa magadisoda katika Bonde la Engaruka kwenye hilo Ziwa la Orboloti na haliko katika Ziwa Manyara na naomba hilo liangaliwe na kusahihishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na suala ambalo Kamati imeleta kuhusu ukamilishaji wa miradi ambayo inaonekana inakwenda kuwapatia wananchi nguvu za kiuchumi na maendeleo. Kwa mfano, wananchi siku hizi wanahamasishwa waanzishe miradi mbalimbali, waanzishe majengo ya zahanati yajengwe mpaka lenta; waanzishe majengo ya shule, madarasa na nyumba za walimu wajenge mpaka lenta na nyumba za madaktari. Inapofikia mahali ambapo wananchi wamekamilisha ile miradi na Serikali ikaendelea kuchelewesha kuja kuwaunga mkono na kumalizia inawavunja wananchi moyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Kamati kwa sababu ni maoni yao na kuisihi Serikali iwekeze katika kuweka bajeti ya kutosha kumalizia miradi ambayo imeanzishwa kwa nguvu za wananchi. Tuna miradi mingi ya mfano ambayo ningeweza kutoa katika Jimbo langu, lakini kwa sababu tunachangia mpango kwa ujumla wake katika kuielekeza na kuishauri Serikali, naomba nisiende huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dakika zilizobakia naomba nielekeze maoni yangu katika kuchangia hili suala la Wakala wa Maji Vijijini. Kwa kweli kama tulivyoanzisha TARURA, naishauri Serikali ifanye haraka kuanzisha wakala huu. Ningefurahi kujua ni lini Wakala wa Maji Vijijini utaanzishwa kwa sababu moja ya vyanzo vya migogoro katika Taifa letu na hata dunia kwa sasa hivi vinatokana na masuala ya ardhi na maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya maji ndiyo yamesababisha kuwa na mgongano mkubwa kati ya jamii zinazoishi katika maeneo yaliyohifadhiwa ambayo ndiyo yenye maji nyakati za kiangazi na maeneo mbalimbali kama Hifadhi za Taifa au Ranchi za Kitaifa. Tukipata wakala huu ukaharakisha kasi ya kupeleka maji katika maeneo mahsusi ya wafugaji, tutaepusha migogoro mingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, katika hili suala la ardhi, naomba pia nidokeze kwa kusema kwamba hii Sera ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambayo inasema kwamba kuna sera ya kupanga, kupima na kusajili ardhi ipewe kipaumbele katika huu mpango wa mwaka wa fedha unaokuja ili kila kipande cha ardhi basi kiweze kupimwa; maeneo ya uwekezaji yaweze kubainishwa na maeneo ya wafugaji na wakulima yaweze kutenganishwa ili kupunguza migogoro ambayo inaendelea kutukabili kila wakati na huenda ikawa ni changamoto moja ya kutopeleka mbele maendeleo ya Taifa letu. Sasa hivi kuna migogoro mingi kati ya vijiji na vijiji, wilaya na wilaya na hata mkoa na mkoa na nafikiri hii sera ya kupima, kupanga na kurasimisha usajili wa ardhi, ingepewa kipaumbele katika mpango wa 2019/2020 tutaweza kupiga hatua kubwa katika kuharakisha kasi ya maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa muda ulionipa, basi naishia hapo.