Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Mapendekezo ya Mpango huu wa Mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilivyosoma kuanzia tu ule ukurasa wa kwanza nikaanza kupata wasiwasi baada ya kuona kwamba miradi ya kimkakati kwa kweli imekuja mingine mipya lakini ile ambayo ilikuwepo siku zote tunaizungumza haijaelezwa kwamba ni kwa nini imeondoka na imefikia wapi katika utekelezaji wake? Siku za nyuma tulikuwa na miradi ya kimkakati kama Mradi wa Makaa ya Mawe Mchuchuma na Chuma cha Liganga; Mradi wa Magadi Soda ya Engeruka; Mradi wa Kiwanda cha Matairi (General Tyre) na Kurasini Logistic Centre. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha kwamba hatujui ni kwa nini sasa miradi hii haipo tena ukweli na taarifa mbalimbali zinaonyesha kwamba hakuna chochote ambacho kimefanyika katika kuikamilisha hii miradi. Miradi hii imechukua pesa nyingi za walipa kodi na nyingine ni mikopo. Kwa hiyo, tungependa sana kufahamu ni kwa nini hii miradi imeachwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine cha muhimu sana ni kwamba ukiiangalia miradi hii kwa karibu ni miradi ambayo kweli ingetupeleka kwenye maendeleo ya viwanda lakini imeachwa. Sasa ni mapenzi tu ya watu ambao wako kwenye madaraka sasa hivi au ndiyo utaratibu wa kuendesha nchi yetu? Napenda nipate maelezo kuhusiana na jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tumekuwa tukizungumza karibu muda wote wa Serikali ya Awamu ya Nne hasa mwishoni juu ya uchumi wa gesi. Leo ukiangalia katika mapendekezo haya sioni namna ambayo tunakwenda kutumia hiyo fursa ya uchumi wa gesi. Hili na lenyewe napenda nifahamu ni nini hasa kilichopelekea hali hii? Sababu ninazozisikia ni kwamba eti sisi kama Watanzania hatutanufaika sana kutokana na mikataba ambayo imekuwepo. Napenda kujua, hivi kweli ni sahihi kuchimbia hiyo rasilimali ambayo tumepewa na Mungu na kuwaachia hao au tukazungumze nao na kuona ni namna gani tutafanya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia fursa ambazo zingepatikana kutokana na uchumi wa gesi, kuna ajira zaidi ya 7,000 kutokana na vile viwanda ambavyo vingeweza kuanzishwa kule kama vya mbolea, cement na vya gesi yenyewe. Yote hayo tumeyakimbia na kwenda kuingia kwenye mambo mengine ambayo kwa kweli mimi siku zote naita ni kucheza kamari kama ule mradi wa ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii vilevile inaacha maswali mengi juu ya Serikali hizi ya CCM. Hivi hakuna mahusiano kati ya Serikali iliyotangulia na hii ya sasa hivi? Au tuamini kwamba hizo Serikali zote zilizopita zilikuwa ni za wapigaji tu na ndiyo zimeifikisha hii nchi sasa inakuwa kama ndiyo inaanza upya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiachana na hiyo, ukweli ni kwamba tungefuatilia uchumi wa gesi na ile miradi mingine ya kipaumbele, leo tusingekuwa tunakwenda kuingia kwenye mgogoro wa kwenda kwenye Stiegler’s Gauge ambapo tunakwenda kugombana na jamii ya Kimataifa. Vilevile sustainability ya huo mradi unaacha maswali mengi, kwa sababu kuna mambo ya mabadiliko ya tabia nchi, pia kuna uchumi wa utalii ambao tunakwenda kuua bila sababu yoyote ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine kwenye hii ni ushirikishaji wa wadau ambao imetamkwa huku, lakini ukienda kuangalia hali halisi sasa hivi ya nchi yetu ni tofauti. Unapozungumza ushirikishaji wa wadau ni pamoja na kushirikiana na jamii ya Kimataifa. Nataka ni-echo hoja aliyotoa hapa Mheshimiwa Mchungaji Msigwa kwamba sisi tumeamua kujitenga na dunia. Kama Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ameamua kutokuhudhuria mikutano yote mikubwa hata ya Umoja wa Mataifa, nafikiri ni lazima sisi kama Bunge tuchukue nafasi yetu, tushauri, tuseme siyo sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama suala ni gharama, ukienda pale UN unakuwa na fursa ya kukutana na viongozi wengine wa dunia kwa kutumia gharama hizo za kukupeleka wewe UN. Sasa kinachotufanya tusiende kwenye Jumuiya ya Madola, tusiende kule Davos ni nini? Hivi sisi kweli tunaweza kuwa kisiwa tukaishi wenyewe tu humu humu ndani kama kuku anaatamia halafu tukaweza kuvuka kweli? Kwa hiyo, naomba sana Bunge lako liangalie jambo hili na kuliwekea utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kushirikisha wadau vilevile ni kuangalia haki kwa wadau, is not one way traffic. Siyo suala la kwamba Serikali inaweza ikafanya tu jinsi inavyotaka kwa wadau. Leo wako wafanyabiashara wakubwa kwenye nchi hii ambao wako ndani kwa visingizio mbalimbali. Siungi mkono ufisadi lakini nafikiri kuna haja ya kuchukua hatua za makusudi wale wote ambao wamewekwa ndani kwa sababu mbalimbali, kesi zao au mashauri yao yafanywe kwa haraka ili waweze kurudi kufanya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumweka ndani mtu ambaye ana uchumi mkubwa kwa maana ya uwekezaji katika hii nchi, maana yake ni kufunga vilevile shughuli zake za kiuchumi. Hii vilevile inawatisha wawekezaji wengine kuingia kwenye biashara na Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye uchumi wa viwanda ambao ni kaulimbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano. Taarifa zinaonyesha kwamba sasa hivi tuna viwanda zaidi ya 52,000, maana hivyo viwanda ukivigawa kwa Majimbo tuliyonayo hapa kila mtu angepaswa aone kwake kuna viwanda kama 300 hivi, lakini kule Moshi Vijijini hatuna kiwanda hata kimoja. Hata ukimwuliza ndugu yangu Mheshimiwa Japhary hapa au ndugu yangu Mheshimiwa Selasini hapa, hatuna viwanda 10. Sasa hivyo viwanda vinajengwa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kwamba Serikali haijengi viwanda bali inajenga mazingira wezeshi kwa ajili ya viwanda kuwepo. Serikali hii imekuwa ikituambia kwamba itafidia yale maeneo ya EPZ na SEZ, itakuwa inatengeneza mazingira mazuri kwa ku-harmonize zile mamlaka za udhibiti, itakuwa inarejesha yale maeneo na viwanda ambavyo vilibinafsishwa lakini havifanyi vizuri lakini kwenye mambo yote hayo ambayo Serikali inapaswa kufanya ni sifuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Halima amesema hapa na akatoa data sana kwenye hiki kitabu cha Hotuba ya Kambi ya Upinzani, ukienda kwenye ule ukurasa wa 70, anasema tulipaswa na Serikali inasema siku zote, tunaweka nguvu kwenye kilimo na mifugo kwa ajili ya kupata malighafi kwa ajili ya viwanda hivi ambavyo tunavipigia debe. Mheshimiwa Halima ametuambia hapa kwamba kwenye kilimo katika mwaka 2016/2017 tumetekeleza bajeti kwa asilimia 2; mwaka 2017/2018 tumetekeleza bajeti kwa asilimia 11. Ukienda kwenye mifugo, tumetekeleza kwa asilimia sifuri mwaka 2017/2018. Pia hizo bajeti hazitoshi, ni finyu, lakini pamoja na ufinyu wenyewe bado tunakwenda kutoa sifuri halafu tunasema tunajenga uchumi wa viwanda. We are joking! Tunafanya utani na haya mambo na tunawatania Watanzania, hatuwatendei haki. (Makofi)