Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza mawazo mazuri yaliyotanguliwa na Wabunge wenzangu hasa wa Chama cha Mapinduzi kwa kuwa wamedhamiria kuweza kuunga mkono na kumtia moyo Rais na jemedari wetu mzalendo namba moja Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mawaziri wote na vilevile pongezi za pekee ziende kwako wewe Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuwa wewe umekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kwamba Mheshimiwa Rais anakwenda kufanya na kutimiza yale aliyoahidi, aliwaambia Watanzania alipokuwa akiomba kura mwaka 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona katika mpango Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kutekeleza yale ambayo Mheshimiwa Rais aliahidi katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015. Nina furaha kuona kwamba katika bajeti ya elimu ni kwa jinsi gani ambavyo Serikali ya Awamu ya Tano na hasa ilivyojidhatiti katika kuhakikisha kwamba elimu ni bure, tumeona kwa jinsi ambavyo hivi sasa idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa katika shule za msingi na sekondari imeongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii pia imewawezesha hata wale wanafunzi ambao kwa namna moja au nyingine hawakuweza kupata elimu wazazi wao hivi sasa wamepata ahueni ya kuwaandikisha watoto wao na ndiyo maana leo hii tunajivunia kwa kuona kwamba idadi kubwa imeongezeka, pongezi za dhati kabisa kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi na mpaka kufikia hivi sasa kwa mujibu wa taarifa ya jana inaonesha kwamba ni bilioni 20.9 ambazo zinatolewa kwa kila mwezi. Utaona kwamba hizi kwa mwaka mzima zinakwenda bilioni 250.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mapendekezo ya mpango tumeona kwamba kuhusiana na suala zima la umeme wa REA ni kwa jinsi gani ambavyo Serikali imeweka nguvu kuhakikisha kwamba wananchi na hasa wa maeneo ya vijijini kuelekea uchumi wa kati wanapata umeme. Tunafahamu umeme na hivi sasa katika suala zima la viwanda umeme unahitajika sana. Jumla ya vijiji 557 tumeona kwamba hivi sasa tayari vimekwishapata umeme huu wa REA na hii itawawezesha wananchi waweze kujikita katika shughuli mbalimbali za uzalishaji mali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni jitihada nzuri za Mheshimiwa Rais wetu ambaye anawapenda na anawapigania wananchi wake kuhakikisha kwamba anatutoa hapa tulipo na kufika katika uchumi wa kati mwaka 2025. Hili ni jambo la kujivunia na nawapongeza tu Mawaziri na Waziri mwenye dhamana ya umeme basi endeleza jitihada hizo na sisi tunakuunga mkono tupo nyuma yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika mabadiliko ya Sheria za Madini tumeona ni kwa jinsi gani zimeongeza pato na hasa katika ujenzi wa ukuta kule Mererani. Kwa mujibu wa taarifa tumeona kwamba hapa ukuta huu ambao una kilometa 24.5 mapato yameongezeka toka bilioni 194.4 kwa mwaka 2015 na kuendelea lakini hadi mwaka 2018 sasa hivi ni bilioni 301.2. hizi ni jitihada njema kabisa za Serikali ya Awamu ya Tano katika kuhakikisha kwamba madini yanawafaidisha wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nasema tu kwamba nimpongeze pia hata katika Bunge la Afrika nilimuona mmoja wa Wabunge kwa kweli Mheshimiwa Silinde nikupongeze umeona jitihada hizi na ukapongeza kwamba kazi nzuri inayofanywa na Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa mabadiliko ya sheria zilizoletwa hapa Bungeni zimewezesha na ukawataka pia Wabunge kutoka Mabunge mengine ya Afrika nao waige mfano kwa Rais wetu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli. Hii ilikuwa ni jitihada na credit nzuri kwa nchi yetu na hongera sana kwa huo uzalendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona ni kwa jinsi gani katika vituo vya afya vimeboreshwa, wananchi wengi maeneo mengi walikuwa hawapati huduma ya afya. Mimi naamini kabisa kwamba jitihada hizi zitakwenda kupunguza vifo vya wanawake na watoto, lakini vilevile wananchi wengi watapata huduma hii kutokana na vituo hivi vinavyojengwa maeneo mengi hakukuwa na hivyo vituo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uamuzi wa Rais kuhakikisha kwamba tunatumia nguvukazi ya wananchi, vituo hivi vimejengwa katika ubora na vilevile gharama zake zimewezesha kupatikana yale majengo yote yaliyotakiwa. Naipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa jitihada hizi kuhakikisha kwamba wananchi wake kwa sababu ili tuwe na uchumi ulio imara tuweze kuzalisha mali tunahitaji afya na kwa wananchi wakipata afya basi uzalishaji mali utaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubali kwamba kutokana na jitihada hizi na vilevile kwamba wenzetu wanasema Serikali imewekeza sana katika vitu, ni kweli tunawekeza katika vitu kwa mfano barabara ili tuwawezeshe wananchi waweze kufika kutoka eneo moja na lingine. Vilevile wananchi hawa wataweza kusafirisha biashara zao na kusafiri wao wenyewe tofauti na hapo awali ilivyokuwa na ndiyo maana leo hii ukitoka Arusha mpaka Tunduma kwenda mpakani mwa Zambia na Tanzania ni barabara ya lami kutokana na jitihada nzuri za Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, tunaona kwamba katika suala zima la kilimo kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu jitihada zinavyofanyika hivi sasa ambapo amekuja na mipango/mikakati ya kuhakikisha kwamba wanawawezesha vijana katika kilimo. Wao wamedhamiria kwa dhati kabisa kuhakikisha kwamba tunaingia katika kilimo cha vitalu (green house). Huu ni mpango mzuri na jitihada zinazofanywa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu ili vijana waweze kujiingiza kwenye kilimo na siyo kwa kufanya hivyo tu. Serikali yenyewe inawawezesha vijana hawa kwa kupitia mikopo mbalimbali ili waweze kujipanua zaidi katika suala zima la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, habari njema ni kwamba na masoko pia tayari kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu wamekwishaanza kuwatafutia vijana hawa. Kwa hiyo, napongeza sana jitihada hizi kupitia kwa Waziri Mkuu, kupitia kwa dada yetu Mheshimiwa Jenista Mhagama na Naibu wako kutokana na kazi nzuri mnayofanya. Nina imani kubwa kabisa na Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile vikundi vya ujasiriamali vimewezeshwa na siyo hao tu, nina furahi sana kupitia sheria ya 442 ambayo itawawezesha makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kupata mikopo na tayari baadhi ya Halmashauri zimekwishaanza kutekeleza hili, hii itatusaidia pia kupunguza umaskini. Pia itatusaidia kupunguza ile hali ya kuwa tegemezi na yote haya ni kutokana na mipango mikakati mizuri iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanasema hakuna usalama, nchi hii ni miongoni mwa nchi ambazo zinaongoza kwa amani. Wenzetu waliopo nchi jirani wanajivunia Tanzania na kuitolea mifano, ndugu zangu tuendeleze amani tuliyonayo na amani hii ndiyo itakayotuwezesha kufika katika uchumi wa kati mwaka 2025. Kwa maana hiyo kwamba kukiwa na amani watanzania wataweza kwenda kufanya shughuli zao mbalimbali za ujasiriamali lakini vilevile kwenye kilimo na shughuli zingine ambazo zitawawezesha wao kuongeza kipato chao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kutokana jitihada nzuri za Mheshimiwa Rais wetu mzalendo namba moja, Rais ambaye katika dunia hii wanamtolea mfano na waswahili wanasema kwamba kwenye miti, hapana wajenzi. Mimi nasema kwamba wajenzi ni sisi wenyewe na ni kutokana na Rais huyo basi atatufikisha katika uchumi tunaoutarajia kufikia uchumi wa kati mwaka 2025. Tumuombee Rais wetu na tumuunge mkono ambaye ameruhusu wajasiriamali waweze kuingia maeneo mbalimbali kujipatia kipato. Hivi sasa hata wizi umepungua kutokana na vijana wengi wanajishughulisha katika shughuli za kujiletea vipato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Wabunge wenzangu tuendelee kuungana na Mawaziri na kumuunga mkono Rais wetu kuhakikisha kwamba yale aliyoyaahidi mwaka 2015 anayafanyia kazi na kuyatimiza. Jambo la muhimu ni kuona kwamba ni kwa jinsi gani amedhamiria miradi mikubwa ya umeme kwa mfano Stiegler’s Gorge na mradi wa reli ambao tayari umekwishaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ssa katika Jiji la Dar es Salaam hata foleni zimepungua kutokana na miundombinu inayojengwa na kwa mfano daraja la TAZARA. Hizi ni jitihada zinazoonyeshwa na Rais wetu kwa kipindi kifupi, tunatarajia kwamba kwa miaka mitano itakayokuja kutakuwa na mafanikio makubwa zaidi na endapo tutaendelea kumuunga mkono. Mungu akupe maisha marefu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, tunakupenda, tunakuhitaji sana na tunaona kwamba wewe umedhamiria kuwakwamua wananchi wako na una dhamira ya dhati kabisa katika kuhakikisha kwamba unatutoa hapa tulipo kufika katika uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.