Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Augustine Vuma Holle (23 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ambayo nimeipata kuingia kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Niwashukuru sana wapigakura wangu wa Jimbo la Kasulu Vijijini kwa kura nyingi sana ambazo wamenipa na kunipa Halmashauri yote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo nimpongeze sana Mheshimiwa Magufuli kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi sana kuwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, lakini na Baraza lake lote ambalo leo hii linachapa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu mimi pamoja na Watanzania wengi tunayo imani kubwa sana pamoja na kasi ambayo mmeanza nayo. Chapeni kazi, longolongo, umbea, majungu, achaneni nayo, fungeni masikio angalieni mbele, pigeni kazi. Mwanafalsafa mmoja aliwahi kusema kwamba; “you cannot carry fundamental changes without certain amount of madness.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo niseme tu, nimepata nafasi ya kusikiliza michango mingi sana pande zote mbili katika kuboresha kitu hiki. Nimewasikiliza Wapinzani, lakini nimeguswa sana sana aliposimama kuchangia Mheshimiwa Lema. Mheshimiwa Lema ameongea vitu vingi sana hapa ambavyo kimsingi vimenigusa, lakini kwa sauti yake ya upole ya kutafuta huruma ya wananchi, imedhihirisha kwamba, yale Maandiko Matakatifu yanayosema kwamba angalieni watakuja mbwa mwitu wakiwa wamevaa ngozi ya kondoo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme, Mheshimiwa Lema amesema sana kuhusu demokrasia. Anadai kwamba Chama cha Mapinduzi kinakandamiza sana demokrasia katika nchi hii, lakini tukumbuke chama chake, mgombea wao Urais mazingira ambayo walimpata, kahamia kwenye chama chake, kesho yake akapewa kugombea Urais, hiyo ndio demokrasia! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwenyekiti wa Chama chao ni yule yule na wakati wa uchaguzi wale wote waliotangaza ndiyo wagombea Uenyekiti walifukuzwa kwanza na uchaguzi ukafanyika je, hiyo ndio demokrasia?
Pia kuhusu Viti Maalum, hakuna chama ambacho kimelalamikiwa katika nchi hii kama Chama cha CHADEMA katika mchakato wa kupata Wabunge wa Viti Maalum hiyo ndiyo demokrasia? Mnataka demokrasia tufuate maslahi ya CHADEMA, hiyo ndiyo demokrasia ambayo mnataka tuje kwenu!
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niendelee kusema tu, wakati Lema anasema alimwambia Mwenyekiti atulie na ninyi nawaambia tulieni mnyolewe.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lema amezungumza kuhusu ugaidi hapa. Naomba nisema ugaidi ni inborn issue ni issue ambayo mtu anazaliwa nayo na sifa zake ni uhalifu na kila mtu anafahamu historia ya Lema hapa. (Makofi)
MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Anasema kwamba, anasema, tulia unyolewe tulia, tulia unyolewe vizuri, tulia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa....
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Wamesema watu hawa kama nchi hii itakuwa na vurugu basi mapato au uchumi wa nchi hii utashuka, lakini kila mtu anafahamu kwamba Arusha ni Mji ambao ulisifika kwa kuwa na amani sana, Arusha ni Mji ambao ulisifika kwa kuwa na uchumi wa hali ya juu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii hapa Mjumbe yule aliyesimama amesema uchumi wa Arusha umeshuka. Leo hii kila Mtanzania anajua kwamba Mheshimiwa Mbunge aliyeko sasa hivi wa Arusha Mjini amekuwa ni chanzo cha kuchafua amani ya Mji wa Arusha na amesababisha uchumi wa Arusha kuporoka kwa kiasi kikubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wanataka twende kwao tukajifunze nini hawa! Tulieni mnyolewe vizuri. Lakini naomba niseme, ndugu zangu lazima tuwe makini sana na niwasihi, Wapinzani ni marafiki zangu sana wengi. Lazima tuwe wakweli na tulitangulize Taifa letu mbele.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Tunapoomba kuchangia, tuchangie katika namna ya kujenga, siyo katika namna ya kubomoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu Mpango huu, mpango huu.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa baada ya kuzungumza hayo, niende kuzungumza yale ya wananchi wangu wa Jimbo la Kasulu Vijijini, dose imeshaingia hiyo.
Suala la kwanza, kwanza niungane na mchangiaji Mheshimiwa Zitto Kabwe kwa alichozungumza hapa, alizungumza kwamba, Kigoma ni miongoni mwa mikoa ambayo imeachwa nyuma sana. Pamoja na Mpango mzuri ule, naomba niseme kwamba kwanza kwa suala la miundombinu, iko barabara ya kutoka Nyakanazi mpaka Kidahwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wote wa Mkoa wa Kigoma wote wanafahamu kwamba hapo ndipo uchumi wa Kigoma umefungwa. Naomba sana Serikali ya Awamu ya Tano, niseme tu kwamba bajeti ijayo kama haitakuwa na barabara hii nitatoa shilingi kwenye bajeti hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, ni kuhusu reli ya kati kwa standard gauge. Reli ya kati ni mhimili wa uchumi wa nchi nzima ya Tanzania, lakini waathirika wakubwa sana ni sisi watu wa kanda ya magharibi. Naomba niseme tu, niungane na wachangiaji wote, tuhakikishe reli hii ya kati inajengwa kwa standard gauge. Narudia maneno yale yale, kama kwenye bajeti tutakapokutana hapa kuja kujadili maendeleo haya, reli hii kama hamjatuletea kwa kinagaubaga tutaijengaje kwa kweli nitatoa shilingi. (Makofi)
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine...
MWENYEKTI: Ahsante sana.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa uhai huu. Kwanza niseme kwamba, naona fahari kubwa sana kuwa Mjumbe wa Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma. Kamati ambayo kwa kushirikiana na Serikali imefanya mambo makubwa, ime-improve vitu vingi sana kwenye mashirika ya umma. Pia nimpongeze Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kuwasilisha vizuri taarifa yetu na nimpongeze pia kwa namna ambavyo anaendelea kuendesha Kamati hii kwa weledi mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza nipende kumpongeza Mheshimiwa Rais yeye mwenyewe kwa kuamua kushirikiana na Mawaziri kuhakikisha kwamba, anasimamia mashirika ya umma kwa ukaribu mkubwa, lakini na weledi wa hali ya juu sana. Usimamizi huu na umakini ambao Rais ameuonesha umeleta mafanikio makubwa sana kwenye mashirika ya umma, ziko chagamoto ndiyo, lakini mafanikio ni makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano taarifa imeonesha hapa na imesema kwamba, Shirika kama TANESCO kwa zaidi ya miaka 20 shirika limekuwa linapata hasara zaidi ya miaka 20 wanatengeneza hasara tupu. Na wamekuwa wanatumia fedha za umma kwa ajili ya kujiendesha, yaani wamekuwa wanapokea ruzuku, lakini kwa mara ya kwanza imetoka kwenye shirika linalotengeneza hasara na kuanza kutoa gawio, limetoa zaidi ya bilioni 1.4 mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama haitoshi Shirika la Madini la STAMICO. Hili nalo tangu lmeanzishwa mwaka 1970 halijawahi kutoa gawio lolote Serikalini, lakini chini ya jembe Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli sasa STAMICO imetoa gawio la shilingi bilioni moja. Kama hiyo haitoshi tumeona uundwaji wa kampuni ya Twiga Minerals, hii sasa ndio baba lao, shirika ambalo limeenda kufanya mabadiliko makubwa sana. Tumeibiwa sana, tumenyonywa sana na vijana wote wa nchi hii, wasomi, wazee, hata ambao hawajasoma kila mtu alikuwa anajua kwamba, nchi hii ilikuwa inaibiwa kwenye upande wa madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapata mwanga mweupe kwamba, kwa mara ya kwanza imeundwa kampuni ambayo tutakuwa tunagawana fifty fifty yaani 50 wao 50 sisi, jambo ambalo ni maajabu kabisa kwenye nchi yetu kwa hiyo, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. Wabezaji watakuwepo tu watabeza, acha wabeze, lakini Watanzania wenye akili timamu wanaona na wanaona kazi kubwa ambayo anaifanya na wako pamoja na yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri kwenye mambo machache. Jambo la kwanza nataka kama alivyosema Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwepo na mabadiliko ya sheria ili tuweze haya mambo ambayo Rais mheshimiwa Dkt. Magufuli anayafanya kwenye mashirika mbalimbali yaweze kuwa sheria. Kwa sababu, leo yuko Rais Magufuli na leo amesema, kesho akinyamaza asiposema au kesho akitoka, tuna uhakika gani kama atakayekuja naye atakuja kusema kama alivyosema Mheshimiwa Dkt. Magufuli?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, wakati anapokea mwaka jana gawio, Mheshimiwa Rais akasema mashirika yote ya umma ambayo hayajatoa gawio leo, akawapa siku 30 nadhani ilikuwa, siku 60, akasema ambao hawajatoa gawio basi bodi za mashirika hayo zimejifuta rasmi. Baada ya kutoa kauli ile ziliongezeka bilioni 20 zaidi, hizi bilioni 20, Mheshimiwa Waziri, Mama Ndalichako anajua, ndizo fedha ambazo zinzenda kutumika kugharamia elimu bila malipo nadhani kwa mwezi ni bilioni 19. Yaani kauli moja tu ya Rais imeenda kugharamikia elimu mwezi mzima nchi nzima. Kwa hiyo, haya mambo tuyafanye sasa kuwa ni sheria kwamba, tufanye mabadiliko ya sheria, sheria isitamke tu kwamba, mashirika yalete gawio, lakini bodi ambazo zitashindwa kuongoza mashirika kuleta gawio ziwe zimejivunja kwa mujibu wa sheria, iwe sheria kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wale ambao watafanya matumizi ambayo hatuyaelewi kwa sababu, matumizi nayo yamekuwa regulated na sheria. Kama wataenda kinyume na sheria kwa sababu yako makampuni mengi na mashirika mengi ambayo wanatumia hela hovyo hovyo tu, sasa lazima tuweke kisheria hii kwamba, wakienda nje ya mfumo wa sheria bodi zenyewe zijivunje na kama haitoshi hata kwenye uwekezaji usio na tija, tumeona NSSF, watu wanaenda kujenga majumba porini huko ambayo hayauziki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuseme haya tuyaweke kwenye sheria kwa sababu, hawa watu najua wanaenda kufanya uwekezaji mbovu wana akili, kwa nini nyumba zao wanajenga mjini, lakini uwekezaji wanaenda kupeleka maporini? Wanajua, washapiga percent zao halafu wanafanya vitu vya hovyo. Sasa lazima Sheria itamke kwamba itoe kwamba mtu anapofanya uwekezaji ambao hauna tija ambao kwa wazi wazi unaonekana kabisa kwamba huu ni utapeli, na zenyewe wawajibishwe, Bodi kuvunjwa na kuchukuliwa hatua za Kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Msajili wa Hazina TR, kwanza nimpongeze Msajili wa Hazina Bwana Mbuttuka amekuwa ni msaada mkubwa sana kwenye Kamati yetu, ametuongoza vizuri sana na kwa sababu amepewa jukumu la kusimamia Mashirika zaidi ya 200 kwenye nchi hii, mimi nadhani anapaswa kuongezewa raslimali watu lakini pia na raslimali fedha, mashirika zaidi ya 200 ya nchi hii huyu Msajili wa Hazina ndiye anayeangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mashirika 256 kwa hiyo lazima aongewe fedha sisi tunajua kazi ambayo anaifanya kule tunajua kwa hiyo aongezewe pesa na raslimali watu ili aende kuyasimamia vizuri mashirika haya ninaamini akiongezewa fedha na raslimali watu tutajua mengi zaidi kwenye Mashirika huko tukishirikiana na Kamati yetu ambayo iko chini ya Jemedari Mheshimiwa Chegeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba suala la sukari, tumekutana na watu wa Kilombero tukaenda mpaka Kiwandani kwao kutembelea. Suala la sukari nchi hii bado kuna jambo la ziada na nimuombe Mheshimiwa Rais, jambo hili aliingilie kati mwenyewe, ukweli ni kwamba nchi hii ya Tanzania ina ardhi kubwa sana ya kuweza kuzalisha miwa ya kutosha, lakini ukweli ni kwamba tunayo nafasi kubwa sana ya kuongeza uzalishaji wa sukari kinachotakiwa hapa ni utashi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wawekezaji wapo, kama tukipunguza bureaucracy kwenye Uwekezaji lakini pia kukatokea msukumo mkubwa wako watu wengi ambao wanaweza wakawekeza kwenye sukari na tukapata sukari ya kutosha kwenye nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo tu-burn importation of sugar, kuagiza sukari nje ya nchi ndiyo kunaleta sukari isiyo na viwango, sukari ya bei ndogo ambayo inakuja kuathiri uzalishaji wa sukari nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nimekuwa naona kwenye maduka wanauza, juzi nimeshangaa kweli, kwenye maduka tunauziwa sukari hii nyeupe hii, kwa ajili ya matumizi, juzi wamekuja wataalamu wanatuambia sukari nyeupe ni sukari ya viwandani, siyo nzuri kwa afya mtu kuunga kwenye chai, lakini tunakula sisi, na wengine wanakula wakidhani sukari nyeupe ndiyo sukari tamu, ndiyo sukari ya premium kumbe wanakula uchafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hayo yote kama tunakuwa tuna uzalishaji mkubwa wa sukari kwenye nchi yetu maana yake tunaweza kupunguza uingizaji wa sukari isiyo na viwango lakini pia tunaamini tutakuwa tunalinda Viwanda vyetu katika nchi, na tutaongeza uchumi kimsingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ninalisema kwa uchungu mkubwa kwa sababu ninaamini tunao uwezo wa kuzalisha sukari kwa kiwango ambacho Taifa hili linahitaji na wakati mwingine mpaka tukafanya exportation kwa sababu ardhi tunayo, Wawekezaji wapo, kinachotakiwa ni utashi na kuweka mazingira mazuri ya Uwekezaji ili watu waje kulima na kuzalisha sukari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kabisa ni kuhusu hawa watu ambao wanakaimu Ofisi, ooohh! muda umeisha nadhani…

MBUNGE FULANI: Bado! Bado! bado.

MWENYEKITI: Malizia sentensi yako ya mwisho….

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, Makaimu hawa ufanisi wao wa kufanya kazi ni mdogo kwa sababu mtu anapokuwa anakaimu nafasi yake confidence ya kufanya kazi inakuwa ni ndogo sana. Kwa hiyo, Mashirika mengi yana watu ambao wana Kaimu tunaomba Mamlaka ili jambo kama tumeweza kuchomoa Wafanyakazi hewa tukafanya hiyo, hili linashindikana vipi kwenye Mashirika haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufanye uchunguzi mzuri wa ambao wanafaa wapewe nafasi zao na ambao hawafai basi waondolewe wapewe watu wengine ili kuondoa suala la kukaimu kuongeza ufanisi kwenye Mashirika ya Umma. Nakushukuru sana naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa jioni ya leo ambayo nimepata na mimi kuungana na wenzangu kwenye kuchangia bajeti hii ambayo ni bajeti inayoonekana inakwenda kumkomboa Mtanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na mambo matatu; jambo la kwanza, nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya bila kuchoka kuweka mikakati vizuri kwa ajili ya maendeleo ya nchi hii kwa ujumla. Dhamana aliyopewa ni kubwa na sisi tunamuombea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kumkaribisha Ikulu pacha wangu, Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Papa Félix Tshisekedi. Sisi watu wa Kigoma uchumi wetu kama Mkoa una mashirikiano makubwa sana na nchi ya Kongo. Kwa hiyo Rais alivyomuita Rais mwenzake wa Kongo kumkaribisha Ikulu tunaamini kwamba wamezungumza mambo makubwa na mazuri ambayo yatapunguza baadhi ya vikwazo mpakani pale na hatimaye tutaendelea kupokea Wakongomani wengi Kigoma kwa ajili ya kufanya nao biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye bajeti; nipende kushauri yafuatayo, jambo la kwanza, upande wa mawakala hawa wa kutoa mizigo bandarini. Kaka yangu Dkt. Mpango, mimi hili sijalielewa vizuri, ninapenda Serikali ije na maelezo mazuri na ya kina tuweze kuelewa kwa sababu tunaamini clearing and forwarding ni profession ya watu ambao wamesoma vyuoni wamemaliza na wana-practice vizuri ili kuweka waraka wa kufanya shughuli hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa anapokuja mtu wa kawaida tu ambaye hana knowledge hiyo wala haelewi hicho kitu, tunapaswa kujua lakini tuelewe hatma ya makampuni haya ya watu ambao wanafanya clearing and forwarding, tuweze kujua kwa sababu kuna ajira nyingi ambazo ziko huko. Mimi nadhani kama kungekuwa kuna matatizo kwa hao ma-agent ilikuwa ni busara zaidi kuwafanyia vetting na kuwaondoa wale ambao hawastahili kuliko kusema kwamba kila mtu aweze kufanya clearing and forwarding ya mzigo wake. Sina maana ya kupinga hili, lakini nataka Serikali ije kunishawishi, iweze kutueleza tuweze kufahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mifugo; mimi nipende kushauri jambo moja, nchi hii imekuwa na migogoro ya wakulima na wafugaji kila siku. Bunge lililopita niliuliza mkakati wa Serikali kupunguza mifugo labda ili kuweza kupunguza migogoro hii kati ya wakulima na wafugaji, lakini nikaona kwamba kupunguza mifugo kwa kweli ni jambo ambalo ni gumu kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninashauri jambo moja kwamba Serikali nadhani inapaswa kutenga vijiji vya ufugaji ambavyo vitakuwa havina wakulima. Yapo maeneo ambayo Mheshimiwa Rais anasema kwamba yamepoteza sifa za uhifadhi, nadhani tutenge vijiji vya ufugaji ambapo wafugaji wote tutawaambia waende kule na watakuwa hawakutani na wakulima. Hii itaweza kupunguza migogoro kati ya wakulima na wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sekta ya Utalii; watu wengi ambao wamewekeza kwenye sekta hii wanalalamika kwamba vibali vya uwindaji ambavyo wanapewa ni vifupi. Kwa hiyo, wanashindwa kufanya uwekezaji wa muda mrefu kwa sababu wanapewa vibali vya mwaka mmoja. Kwa hiyo, nashauri Serikali ilitazame hili, itoe vibali vya muda mrefu ili wawekezaji hawa waweze kutoa hela zao mfukoni kufanya uwekezaji kwenye maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano sisi pale Kagerankanda tuna mwekezaji wa kitalu cha uwindaji, alitaka atujengee mabwawa ya samaki kwa ajili ya ile jamii inayozunguka, lakini mradi ule unaenda miaka miwili na ana kibali cha mwaka mmoja kutoka Serikalini. Kwa hiyo amesitisha kwa sababu inawezekana akianza kujenga ule mradi kibali chake kiki-expire basi asiweze kuongezewa na hatimaye akapewa mtu mwingine kwa hiyo inakuwa ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kushauri ni kwenye upande wa hawa…

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Taarifa, taarifa.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: …upande wa elimu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Vuma, kuna Taarifa. Mheshimiwa Mchungaji Peter Msigwa.

T A A R I F A

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka nimpe taarifa mchangiaji kwamba katika jambo analolisema kwamba wawindaji wanapewa vitalu muda mfupi, ninataka nimuongezee taarifa kwamba kwa kweli limekuwa ni tatizo na hivi sasa Wizara ilitoa mpango wa mnada, mnada umeshindikana, kwa hiyo hivi vitalu kuna uwezekano wa kuvipoteza na tukapunguza mapato kwenye mpango wako Mpango kwa sababu mpango huu wa kunadisha vitalu karibu 90 vimekosa wateja, ni mipango mibovu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka nimpe taarifa tu katika hili analolisema.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Vuma, unapokea taarifa hiyo?

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa naipokea na Serikali ije kutoa majibu hapa wakati wa majumuisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye upande wa elimu hakuna…

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa elimu napenda kushauri jambo moja…

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Vuma kuna taarifa kutoka Mheshimiwa Constantine Kanyasu.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninaomba nimheshimu sana Mheshimiwa mchangiaji, lakini ninataka tu niweke kumbukumbu sawa. Mnada ambao unaendelea sasa wa vitalu haujafungwa na mnada huo umepandisha thamani ya kitalu kutoka dola 60,000 kwenda dola 150,000 na ninataka kumhakikisha Mheshimiwa Mbunge kwamba katika marekebisho yetu ya Kanuni suala la mwaka mmoja halipo, tulikuwa na miaka mitano tunakwenda miaka kumi. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Augustine Holle Vuma unapokea Taarifa hiyo?

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa na ninawatakia utekelezaji mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Nabu Spika, niseme kwenye suala la elimu; hili nashauri kitu kimoja; hapa mtaani kuna vijana wengi ambao tumewakopesha fedha nyingi sana ambao wamemaliza vyuo, sisi tunawadai pesa, lakini wao wanaidai Serikali ajira na wakati huo huo Serikali haina watumishi wa kutosha kwenye idara za walimu, katika hospitali na sekta zingine. Sasa nikasema, kwa nini hawa vijana ambao wanamaliza shahada zao ambao wana mikopo, kwa nini tusiwape mikataba mifupi ambayo tutakuwa tunawapa hela za kujikimu na hatimaye waende kufundisha au kufanya kazi katika hospitali huko na kwenye sekta mbalimbali huku wakiwa wanalipa madeni ambayo wanadaiwa na Bodi ya Mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu wale vijana tunawadai pesa, wao wanatudai ajira na hatuna watumishi. Sasa tuangalie sehemu ambayo tutakutana hapo katikati; vijana hawa wakimaliza wakienda kufanya kazi kwanza watakuwa wanalipa madeni yao, lakini pia watakuwa wanapata uzoefu. Kwa sababu vijana wengi wako mtaani, lakini uzoefu wa kufanya kazi hawana mpaka wanashindwa kupata kazi kwenye sekta binafsi kwa sababu hawana uzoefu, kwa hiyo tutawapa uzoefu lakini pia watakuwa wanalipa madeni yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali barabara ya kutoka Buhingwe – Kasulu – Nyakanazi, naomba sana utekelezaji wake. Lakini pia naomba barabara ya kutoka Kasulu kwenda mpaka Uvinza.

Mheshimiwa Naibu Spika, niweze kuja kwenye suala la SGR; nimemsikia ndugu yangu, kaka yangu hapa, Mheshimiwa Mwakajoka anasema kwamba wao hawapingi miradi ya SGR na Stiegler’s Gorge lakini hawataki fedha nyingi ziende kwenye miradi ile; kituko kabisa hiki, hiki ni kituko, yaani miradi unaitaka lakini hutaki fedha nyingi ziende kwenye miradi ile kwa sababu miradi ya matrilioni inatengewa mabilioni…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: …kila mwaka wewe hautaki hela ziende kule ila miradi unaitaka…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: …yaani unajitekenya halafu unacheka mwenyewe. Sasa hili ni jambo ambalo ni la kusta… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Vuma, kuna taarifa. Waheshimiwa Wabunge, hii ni taarifa ya mwisho kwa Mheshimiwa Vuma kwa sababu hii ni taarifa ya tatu tayari. Mheshimiwa Mwakajoka.

T A A R I F A

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka kumpa taarifa mzungumzaji, siyo kwamba tumesema kwamba hatupingi halafu fedha nyingi zimekwenda kule. Tulichokizungumza hapa ni kwamba maeneo ambayo wananchi wengi wanatakiwa kupata huduma fedha hazijapelekwa.

Kwa hiyo, tulikuwa tunaishauri Serikali muda wote na tumeishauri Serikali muda wote kwamba fedha zipelekwe katika maeneo hayo; ndege, umeme, kila kitu tunakihitaji, lakini fedha ni nyingi mno ndiyo maana tumesema tunahitaji mgawanyo ambao uko sawa kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine ni kwamba haja...

NAIBU SPIKA: Taarifa ni moja Mheshimiwa Mwakajoka. Mheshimiwa Augustine Holle Vuma unapokea taarifa hiyo?

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, hii taarifa siipokei kwa sababu huyu mtu anajichanganya na niseme, unajua sisi Mkoa wa Kigoma unapozungumza reli ni identity yetu, ni utambulisho wetu, ndiyo maana Mkoa wa Kigoma umekuwa unaitwa kwamba ni mwisho wa reli. Kwa hiyo, sisi Kigoma tunahitaji reli kwa gharama yoyote ile na ninaishauri Serikali iendelee kupeleka pesa kwenye SGR ili tupate reli, SGR ifike Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua kuna watu hapa ambao kwao wanakotoka maeneo yao hakuna shida za usafiri, wao zimeshaisha. Sasa Kigoma unapokwenda kupinga reli tunakuita ni msaliti wa Mkoa wa Kigoma, kwa hiyo sisi tunaiunga mkono kabisa Serikali, tunahitaji SGR Mkoa wa Kigoma kwa sababu tunaamini itakuwa ni mkombozi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme tunaamini kwamba SGR hii ina faida za muda mfupi katika ujenzi wake lakini na faida za muda mrefu. Faida za muda mfupi, jambo la kwanza SGR hii Lot One na Lot Two inayoendelea kujengwa imeajiri sasa hivi mpaka leo tunavyozungumza Watanzania 17,000 wamepata ajira kwenye SGR. Lakini kama haitoshi kumejengwa kiwanda cha mataruma kwa hiyo unavyozungumza ujenzi wa SGR hauzungumzii vile vyuma kutandikwa peke yake, kuna element ya viwanda kwenye ujenzi wa SGR. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama haitoshi kuna kuchochea uchumi ndani ya SGR; niseme tu kuna watu wengi sana wanafanya shughuli za kimaendeleo wakati mradi ule unajengwa. Ukiangalia kwa mfano vifaa ambavyo mradi ule unatumia ukianzia na cement, inakadiriwa kwamba Lot One na Lot Two itatumia mifuko milioni 9.2 ya cement ambayo yote inanunuliwa hapa Tanzania; lakini itatumia nondo kilo zaidi ya milioni 100, yote inanunuliwa Kamal hapa hapa Tanzania. Sasa ukiangalia haya yanaendeelea kuchochea uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukiangalia bodaboda, mama lishe ukienda kwenye mradi huu wamejaa wanafanya shughuli zao za kiuchumi, huku ni kuchochea uchumi. Kwa hiyo, unavyoangalia reli, ujenzi wa SGR usi-focus kwenye kutandika vyuma tu, kuna vitu vingi viko ndani yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nadhani kuna suala la uelewa; watu wengi huu mradi hawauelewi vizuri, wanausoma na kusikia tu michango ya Bungeni, wanasoma kwenye whatsApp na wapi, wanapaswa waende kutembelea mradi huu waweze kuona au ije presentation Bungeni hapa watu waweze kupewa shule juu ya Mradi wa SGR ili waweze kuelewa kilichopo ndani yake, ule ni zaidi ya mradi wa reli kuna vitu vingi vilivyopo ndani yake; hizo ndiyo faida za muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zipo za muda mrefu; tunaamini kwamba Mradi wa SGR, reli ikikamilika itakwenda kuongeza thamani ya mazao katika nchi yetu. Kwa sababu tunaamini, kwa mfano Mchina amekuja akatangaza soko la muhogo, Kigoma tunalima muhogo lakini gharama za kusafirisha muhogo kutoka Kigoma kuupeleka mpaka bandarini uende China ni very expensive. SGR itakapokuwa imekamilika tunaamini muhogo utatoka Kigoma mpaka Dar es Salaam kwa muda mfupi na gharma zitakuwa chini. Na study inaonesha SGR itapunguza gharama za usafiri kwa asilimia 40; nani anapinga SGR na kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama hiyo haitoshi, tunaamini kwamba itaweza kulinda barabara zetu ambazo tumezijenga kwa gharama kubwa. Mizigo mingi mikubwa itakuwa inapitia kwenye reli hii ambapo itaweza kulinda barabara zetu kwa sababu barabara zitabaki zinatumiwa na magari machache, mizigo yote itakuwa inasafirishwa kwenye treni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nipende kuwaomba kwamba wajitahidi kusoma huu mradi wa SGR. Na niseme; hizi bajeti mbadala hizi ambazo zinakuja na vijembe, zinapinga miradi mikubwa kama SGR ni za kuchana hizi, hakuna kitu. Lazima tuwe serious katika mambo kama haya ili watu waweze kuelewa kwamba… [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

(Hapa Mhe. Augustine V. Holle alichana kitabu cha hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, Kuhusu Utaratibu.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: …hili jambo ni jambo ambalo sisi watu wa Kigoma tunahitaji lifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, Kuhusu Utaratibu.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, Kuhusu Utaratibu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwakajoka umesimama na Mheshimiwa Esther Matiko amesimama na mnazungumzia utaratibu. Mheshimiwa Mwakajoka.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kuna mambo ambayo yanafanyika ndani ya Bunge...

Mheshimiwa Naibu Spika, Kuhusu Utaratibu, natumia Kanuni ya 64; mambo ambayo hayakubaliki.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchangiaji aliyekuwa anachangia sasa hivi amesimama hapa amechana hotuba ya Upinzani ndani ya Bunge hili. Ninafikiri jambo hili ni dharau kubwa lakini pia ni kutokujielewa kwa Mheshimiwa Mbunge kwamba yuko humu kwa sababu gani na hajui kwa nini hiki kitabu amepewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba meza yako iweze kutoa sababu na ni namna gani huyu Mheshimiwa Mbunge asiyejielewa achukuliwe hatua ili kidogo akili yake ikae sawasawa maana yake tumemuona kama kichaa fulani hivi ndani ya Bunge. Ahsante sana. (Kicheko)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tusikilizane.

Amesimama Mheshimiwa Mwakajoka akaitaja Kanuni ya 64 kwamba ndiyo ambayo imemfanya asimame japokuwa ufafanuzi wake haukuwa hasa kwenye kifungu kipi cha Kanuni ambacho anaona kimevunjwa. Lakini Kanuni hii ya 64 Waheshimiwa Wabunge, yako mambo mbalimbali ambayo yanakatazwa na inazungumzia kwa ujumla wake mambo yasiyoruhusiwa Bungeni. Sasa ukisoma Kanuni hiyo ya 64(1)…

Waheshimiwa Wabunge, tusikilizane, huwa napenda kusikilizwa na kwa mujibu wa Kanuni zetu nikiwa nimesimama mnapaswa kunyamaza ili mjue nasema nini.

Kanuni ya 64(1) ukiisoma (g) inazungumza kuhusu kutokutumia lugha ya kuudhi au inayodhalilisha watu wengine. Kwa hiyo kwa mchango wa Mheshimiwa Vuma, hoja iliyopo itakuwa si kuchana kitabu maana amezungumza wakati akichana kitabu.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Vuma kwa muktadha wa Kanuni hii ya 64(2) ukizisoma zote kwa pamoja, Mheshimiwa Vuma maneno ya kuhusu kukichana kitabu hicho nitakupa fursa ili uweze kuyafuta na jambo hili Waheshimiwa Wabunge lisirudiwe wakati mwingine.

Mheshimiwa Vuma.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, napokea busara za Kiti, nafuta maneno yale. Lakini ilikuwa ni kuonesha namna gani ambavyo hotuba hii haina maslahi kwa umma. Ahsante sana.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai mpaka leo, lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango huu wa Maendeleo ya Miaka Mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na zao la chikichiki. Zao la chikichi kwetu Kigoma ni utambulisho wetu, ni identity yetu, ukitaja chikichi ama mawese Tanzania hii kwa watu inakuja ya Kigoma picha, lakini chikichi kwetu ni ajira lakini pia chikichi ni siasa. Sasa nimesoma Mpango huu wa Miaka Mitano vizuri sana, ni mzuri kwa kweli, lakini niseme tu, nchi hii mahitaji yake ya mafuta kwa mwaka ambayo tunaagiza kutoka nje ni jumla ya tani 570,000 kwa mwaka bado kwa mujibu wa takwimu ya Serikali. Watanzania wanahitaji mafuta tani laki 570,000 kwa mwaka, lakini ambayo tunazalisha sisi Tanzania ni tani 205,000 peke yake. Maana yake tunaagiza kutoka nje tani 365,000. Zaidi ya asimilia 50 ya mafuta ambayo tunatumia sisi watanzania tunaagiza kutoka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba katika huu Mpango wa Miaka Mitano, Serikali ijikite kuweka malengo ya kuhakikisha kwamba tunaweza kuzalisha mafuta ambayo tunaweza kulisha watanzania pasipo kuangiza nje na inawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye matunda yanayotoa mafuta, tafiti inaonesha mchikichi ni namba moja, zao namba moja kwenye matunda yanayotoa mafuta. Ziko ripoti zinazoonesha, wapo waliokuja kwenu Tanzania wakachukua mbegu za michikichi, wakaenda kwao, leo hii wanatumia yanawatosheleza mpaka mengine wana-export kwenda nje ya nchi. Sasa ushauri wangu kwa Serikali kwanza nimshukuru Waziri Mkuu kabisa kwa moyo mkunjufu kwa namna alivyovalia njuga suala la kufufua kilimo cha michikichi na kupendeza katika Mkoa wa Kigoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuja mara kadhaa kwa miaka ile ya kwanza, akasisitiza akatoa maelekezo ambapo hamasa imekuwa kubwa sasa, lakini pia kuna mbegu mpya tumepata na kuna chuo kizuri sana kwa ajili ya utafiti wa michikichi kipo. Sasa wananchi wamehamasika wamepanda chikichi kwa wingi sana. Sasa kinachofata hapo ni kwamba wataalam wanasema inawezekana baada ya miaka mitatu minne uzalishaji wa mafuta ya mawese uka-triple yaani ukawa mara tatu. Sasa hofu yangu ni moja tu, tunapoenda kuongeza uzalishaji wa mafuta ya mawese, tumejipanga vipi kisaikolojia ili kuhakikisha kwamba tunaweza kuboresha au kuongeza thamani ya mawese ili yasiliwe Kigoma peke yake yaje kuliwa Dodoma pamoja na mikoa mengine na hata nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mawese kwa asili tunatumia kwenye chakula, sisi watu wa Kigoma, lakini kwa sababu yanakuwa kama crude oil, watu wengine wanakuwa hawawezi kuyatumia. Sasa ukiongeza uzalishaji kama mara tatu, kama hatujajiandaa kuyatengeneza yaweze kutumiwa na watu wengi kwa maana ya kutanua soko, nina uhakika Mkoa wa Kigoma leo hii dumu moja ni Shilingi elfu kumi. Itaenda kushuka mpaka iende elfu tano elfu mbili. Kwa wale wananchi tuliokuwa tunawahamasisha walime mawese, michikichi wataanza kutupiga mawe kwa sababu mawese ni mengi, lakini hatujatanua soko la mafuta yatokanayo na michikichi ili walaji wawezi kuwa wengi. Kwa maana hiyo mengi yatakuwa Kigoma, utashangaa dumu kutoka elfu kumi itaenda mpaka elfu mbili au elfu tatu na kitakachotokea hapo wananchi wataanza kuichukuia Serikali yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ushauri wangu katika hili, ni lazima sasa Serikali kupitia Waziri Mkuu ambaye kwa kweli amekuwa ni rafiki yetu Mkoa wa Kigoma katika hili, tuanze kujielekeza kwenye kuwekeza kwenye teknolojia, tuanze kubuni teknolojia ndogondogo za kuweza ku-refine mafuta ya mawese. Kwa kufanya hivi tutaongeza soko la mawese na hata uzalishaji utakapokuwa umeongezeka, tunaamini kwamba wananchi wataendelea kuuza kwa bei ambayo ni nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukipiga hesabu mafuta ya mawese dumu moja kama nilivyosema ni shilingi elfu kumi, lakini mafuta ya alizeti ambayo ni refined ni shilingi elfu 35 yaani ni sawasawa lita moja ya mawese unauza shilingi 2000 au chini ya hapo, lakini lita moja ya alizeti unauza zaidi ya Shilingi 7000, maana yake nini? Ukifanya double refine kwenye mafuta ya lita tano labda let say unaondoa uchafu labda wa robo lita tu. Kwa hiyo unaweza ukaona namna gani ambavyo wananchi wa Kigoma bado tunanyonywa kutokana na teknolojia mbovu na duni kwenye zao la chikichi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana maelekezo yatoke, SIDO wafanye ubunifu wa teknolojia ndogo ndogo ambazo watu wanaweza kumudu hata wananchi wa kawaida. Kama viko viwanda vya ku-refine alizeti vya milioni kumi, milioni nane, kwa nini Kigoma ishindikane, kwa nini mawese siku zote yaonekane yana rangi nyekundu. Tunahitaji teknolojia ambayo ni ya bei nafuu ili wananchi hata wa kawaida waweze kununua milioni kumi, milioni nane, waweze ku-refine mafuta ya mawese na waweze kuuza kwa bei nzuri na rafiki kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka nizungumzie kidogo kuhusu reli ya SGR. Nashukuru tumeona mipango ipo clear na kwenye bajeti tunaona reflection kuanzia Dar es Salaam, mpaka Mwanza. Sasa ni zamu ya Kigoma; route ya kutoka Tabora kwenda Kigoma, ni ukweli usiopingika ukiangalia mizigo inayopita kwenye reli ya kati kwenda Mwanza na inayopita reli ya kati kwenda Kongo, ya kwenda Kongo ni mingi zaidi na kwenda Kongo unapitia Kigoma. Kwa hiyo tunachotaka na sisi kwenye hii miaka mitano, tumeona kuna mambo mengi sana, lakini nasi tunahitaji tuone kwenye makaratasi na kwenye bajeti ni kiasi gani kinatengwa kila mwaka au ujenzi wa SGR kwenda Kigoma sasa uanze.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesubiri, sasa ni zamu yetu, tunasubiri ikifika Mwanza tu na sisi tuanze kudai. Sasa Mwanza tumeona mpaka mikataba imeanza kusainiwa, juzi tumeona Waziri yupo kule, sasa na sisi Kigoma ni zamu yetu, tuone mikataba ikisainiwa, reli ijengwe kwenda Kigoma, it is our time now.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni la umeme. Kigoma sisi hatujaunganishwa na grid ya Taifa, ni miongoni mwa mikoa michache sana ambayo haijaunganishwa na grid ya Taifa, hii miaka mitano tunahitaji kuona sio story tena, mama ametupa msemo mzuri, ukinizingua nakuzingua, tunakaa humu ndani miaka mitano kwenye bajeti, Mawaziri tunawaomba wakajipange vizuri, Serikali ikajipange vizuri, tunahitaji kuona umeme wa grid ya Taifa unafika Kigoma sio ahadi tena, tutasubiri mpaka lini? Tunaposema viwanda vidogovidogo vije hivi, vinahitaji umeme, sasa kama hakuna grid ya Taifa, umeme wa jenereta wa kuwasha tu, viwanda vinakuwaje? Kwa hiyo tunaomba Serikali ijipange vizuri sana ili tupate umeme wa grid ya Taifa haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sitakuwa nimetenda haki kama sitazungumzia michezo katika nchi hii. Napenda sana michezo, licha ya kuwa Mwanayanga mzuri sana, nawapoongeza Timu ya Simba kwa ilipofika kwa kweli; imejitahidi sana. Na sisi Serikali tuna tabia ya kuvizia mafanikio binafsi ya timu, sisi tunadaka, hata kama ni mazingira mazuri ya Serikali, kwa nini Simba peke yake? Kwa nini nyingine zisifike level hiyo ya Simba? Tuweke vizuri mikakati yetu kwenye upande wa michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na sehemu ya kuanzia, twende kwenye sheria za adhabu mbalimbali za TFF. TFF wana sheria kali kuliko hata za Kanuni za Bunge hili; wana sheria kali kuliko hata za ubakaji. Yaani leo hii Masau Bwire akiwa- challenge kidogo wanamfungia miaka mitano, sasa utafikaje kwenye nani? Uki-challenge kidogo, milioni tano, milioni moja, milioni ngapi; hatuwezi kwenda hivyo. Lazima waweke mazingira vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda michezo sana. Na nimekuwa Mjumbe wa Bunge Sports Club kwa miaka sita sasa. Na hata jana wakati Mheshimiwa Spika alivyotangaza kwamba fomu zinaweza kuchukuliwa, nilichukua fomu kabisa ya kugombea Uenyekiti wa Bunge Sports Club. Kwa hiyo, naamini muda ukifika hata wewe – kwasababu amesema wewe utakuwa msimamizi wa uchaguzi – muda ukifika ntaomba kura.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tujikite vizuri sana kwenye suala la michezo. Michezo ni ajira. Na kweli mimi kama ntapata nafasi hiyo ntaonesha mfano kwenye michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe tu jambo lingine moja, nimeona kwenye ujezi wa miundombinu, hasa barabara… ya kwanza, ya pili hiyo?

NAIBU SPIKA: Ya pili.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Naomba kura yako.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru kwa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye hoja zilizopo mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini na Mkoa wa Kigoma kwa ujumla kwa mambo mengi ambayo anayafanya, to be specific, mambo makubwa matatu: Jambo la kwanza ni ujenzi wa barabara za kiwango cha lami kwenye Mkoa wa Kigoma unaendelea kwa kasi kubwa sana, hizo ni barabara mbalimbali, pia ujio wa Umeme wa gridi ya Taifa katika Mkoa wa Kigoma ni historia kubwa na ya kuenziwa. Pia mpango wa kujenga SGR kuelekea Kigoma ambao bado upo kwenye hatua ya manunuzi ni jambo la kujivuna na la kihistoria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo nitaenda kwenye hoja ambazo ziko mezani. Kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja zote. Baada ya hapo nianze na Benki ya Kilimo. Naanza na Benki ya Kilimo kwa sababu asilimia kubwa ya Watanzania wamejiajiri kwenye sekta ya kilimo, hii ni sekta ambayo inabeba Watanzania walio wengi kuliko sekta yoyote ile.

Mheshimiwa Spika, mwaka huu kwenye bajeti tulitenga Bilioni zaidi ya 700 kwenye bajeti ya Kilimo ukiondoa Bilioni 150 ambazo zimetolewa kama ruzuku. Tume ya Umwagiliaji tulitenga zaidi ya Bilioni 361, sasa ukiangalia Wizara wamejipanga vizuri kuweka miundombinu vizuri sana kwenye upande wa umwagiliaji na sehemu zingine. Wanaweza wakajenga miundombinu vizuri kwa maana ya umwagiliaji, wao hawatalima wataenda kulima wakulima, lakini wakulima wetu hawa wa Tanzania uwezo wao wa kifedha ni mdogo mno.

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya benki nyingi zinatangaza kwamba zinakopesha wakulima lakini hazifanyi hivyo, benki nyingi hazikopeshi wakulima. Ni Benki moja tu ya Kilimo ndiyo ambayo imefanya kwa vitendo kuwakopesha wakulima kiwango kikubwa cha fedha, wengine wanafungua dirisha lakini ukienda wanakuambia hatujaanza kutoa mkopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nina ushauri, katika hizi Bilioni 361 ambazo zimetengwa kwa ajili ya umwagiliaji, kwa nini tusipeleke Bilioni 250 kwenye umwagiliaji halafu Bilioni 100, tukaenda kuwapa hawa TADB - Benki ya Kilimo ili wakulima kama Serikali ikiweka miundombinu vizuri, wakulima wawe na uwezo wa kwenda kukopa ili waweze kuendesha kilimo, otherwise unaweza ukajenga mifumo vizuri, miundombinu mizuri ya kilimo lakini baadae wakulima sasa wakawa wako weak halafu ikawa ni white elephant.

Mheshimiwa Spika, nitaenda kwenye zao la pamba. Mwaka 2019 kidogo tuingie kwenye mkwamo kwenye zao la pamba, nakumbuka vizuri ulikuwa Naibu Spika, wakati ule zao la pamba lili-drop sana duniani na tulikuwa tunaelekea kwenye uchaguzi, presha ilikuwa ni kubwa sana Kanda ya Ziwa, Wabunge wa kule walikuwa matumbo joto. Hivi inakuwaje, inakuwaje! Pamba hainunuliki huko chini. Serikali iliwaita wafanyabiashara wa pamba, tena ambao karibia wote ni Watanzania. Ilivyowaita iliwapa assurance kwamba wanunue pamba kwa bei elekezi ya Serikali halafu Serikali itaenda kuwa- compensate au kuwapa ruzuku. Mpaka tunavyoongea hivi toka 2019 mpaka leo 2022 hawa wafanyabiashara wanadai zaidi ya Bilioni 21. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kutengeneza mjasiriamali Mtanzania ambaye ataenda kwenye level hiyo ya kuombwa na Wizara aweze kunusuru hali, siyo kazi ndogo! Hawa waliopo wachache Watanzania tujaribu kuwalinda na kuwatetea. Serikali inapata kigugumizi gani cha kuwalipa fedha zao? Wakati wanawaita Serikali ilitumia maneno mazuri sana ambayo ni very promising, sasa kwenye utekelezaji, yaani kukopa ni furaha halafu kulipa ni matanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa iko sababu na iko hoja, lazima Serikali ichukue hatua. Tulipata nafasi ya kukaa na Wizara ya Fedha na Mipango na Wizara ya Kilimo, wanasema ooh! kuna vikao. Mimi nasema kama hawa watu walivyoitwa 2019 na wao wangesema ngoja kwanza tuna vikao, mwaka wa kwanza kikao, mwaka wa pili kikao, tungeendelea na benki yetu, hivi nani angeweza kutuondoa kwenye huo mkwamo? Iko sababu ya msingi na iko hoja ya haraka hapa, Serikali ihakikishe inalipa madeni hayo haraka iwezekanavyo ili kuweza kutowaingiza kwenye mgogoro wa kiuchumi hawa wafanyabiashara wetu wa Kitanzania wazalendo, ambao walitutoa kwenye mkwamo wakati ule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzangu wa Kamati yangu wamezungumza suala la mwingiliano kwenye taasisi hizi ambazo tunazisimamia Kamati ya PIC, tunalo Shirika la Marine Services ambalo zamani ilikuwa chini ya TPA lakini sasa hivi ni linajitegemea lenyewe, ziko mali za marine services nyingi ambazo TPA wanazing’ang’ania ziko kwao, inaifanya marine service iwe weak ishindwe kuwa na kipato kizuri, ishindwe kupanga mambo yake vizuri kwa sababu mali zake nyingi zimeshikiliwa na TPA.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilete hapa, kama ni point za kisheria tuweze kufanya mabadiliko ya kisheria ili marine service wapewe mali zao waweze kujengeka vizuri. Walikuja kwenye Kamati wanalalamika, wanaomba msaada.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kuhusu bodi za mashirika mbalimbali. Kwanza mimi na-discourage sana kuwa na bodi hizi za ushauri. Mimi nadhani ni vizuri, na kwa taasisi kubwa kama TANROADS, TANROADS ambayo kila mwaka tunawapa ma-trilioni ya shilingi hapa, lakini wana bodi ya ushauri tu. Ipo tofauti kati ya bodi ya ushauri na independent board. Hii bodi ya ushauri sana sana ni kumshauri Waziri tu basi, lakini hii independent inao uwezo wa kupanga vitu na kuvisimamia bila kuingiliwa na mtu yoyote.

Mheshimiwa Spika, sasa kuwa na hizi bodi za ushauri kwenye taasisi nyeti kama hizi hiyo kwanza mimi na- discourage sana. Hata hivyo, lipo suala la ucheleweshaji wa uteuzi wa bodi. Mimi nakumbuka Machi Mheshimiwa Rais alikuwa anapokea ripoti ya CAG, CAG akasema kwamba yako mashirika mengi ambayo hayana bodi. Mheshimiwa Rais alishtuka pale, akasema mimi nikiletewa kila kitu pale huwa hakikai hata siku mbili au tatu.

Mheshimiwa Spika, sasa ziko bodi nyingi ambazo zimekufa miaka mitatu au minne. Kuna sheria fulani hivi wanasema eti bodi ambayo ina zaidi ya watu 10 ikiisha muda wake eti majukumu yale anachukua Katibu Mkuu wa Wizara. Yaani Katibu Mkuu wa Wizara kichwa kimoja kianze kubeba vichwa 10 vya bodi nzima? ni mambo ya ajabu kabisa.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo bado amepewa mwaka mmoja kwa mujibu wa sheria, hata huo mwaka unaisha bodi haijateuliwa. Sasa nashindwa kuelewa kwamba nchi hii Tanzania kweli hatuna wajumbe wa bodi, watu milioni 61 hatuna wajumbe wa bodi na wenyeviti wa bodi ambao wanaweza waka-fit kwenye hizi taasisi ambazo hazina bodi?

Mheshimiwa Spika, ninaomba, kama tunataka kunusuru mashirika yetu ni lazima tuhakikishe kwamba tunapata bodi kwa wakati. Kwa sababu bila kuwa na bodi, tumeona mashirika yenye bodi na yasiyo na bodi utendaji wao ni tofauti kabisa.

Mheshimiwa Spika, lakini, baada ya kupata bodi, hata hao wenye bodi ukiangalia hakuna mfumo imara wa uwajibikaji. Shirika kupeleka gawio Serikalini yaani ni mpaka wajisikie. Hakuna sheria ngumu ambayo inawalazimisha kupeleka gawio; na ndiyo maana akisimama Mheshimiwa Rais akiwakaripia akitoa tamko kali kuhusu kupeleka gawio, gawio linapanda, asiposema gawio linashuka. Hatuwezi Kwenda namna hiyo, lazima tuweke utaratibu mzuri wa kisheria.

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Kairuki ulivyompa muda wa kusalimia, akasema anaweka mifumo mizuri wizarani pale ili hata akiondoka yeye, ibaki inafanya kazi. Sasa hata hizi bodi zetu hizi lazima tuziwekee utaratibu ambao utawalazimisha, kwamba mkishindwa kufikia level hii ya mafanikio kwenye shirika fulani basi bodi ivunjwe. Hata utaratibu wa kupata hawa watendaji wakuu wa mashirika tunaweza tukawaangalia pia.

Mheshimiwa Spika, tunaweza tukaweka utaratibu, mtu anatakuwa Mkurugenzi wa TANESCO ruhusu watu waombe, watu waombe ukurugenzi wa TANESCO halafu Mheshimiwa Rais apelekewe majina ateue; maana inawezekana labda ukateua mtu labda hataki. Maana kuna mtu mwingine unamwita kwenye Kamati, anakuja pale unaona yaani nia ya ndani ya kusaidia shirika hana kabisa, yupo tu pale anakula posho basi. Ukimuuliza mpango mkakati hana, kama ipo haitekelezeki, yaani hasaidii chochote Serikali. Mimi nadhani tuunde utaratibu waombe hawa watu, tutafute watu competent, waombe, wakishaomba baadaye apelekewe Mheshimiwa Rais kwa mamlaka yake ateue. Haya mambo wakati mwingine, maana tuko watu wengi kidogo…

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa nani kasimama, Mheshimiwa Mtaturu, Mheshimiwa Vuma Holle kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mtaturu.

T A A R I F A

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba ni jambo zuri kuwa na bodi katika mashirika, katika taasisi kwani bodi hizi zina nafasi kubwa sana katika kutoa ushauri. Naomba achukue taarifa kwamba taasisi imara kama za Simba zina bodi ambayo inaongoza mambo mazuri.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa taarifa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Vuma Augustino Holle unapokea taarifa hiyo.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Spika, naomba niendelee. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mimi nashauri mmoja, kama utaratibu wa kupatikana kwa bodi umekuwa ni mgumu kidogo pale ambapo bodi zimemaliza muda wake, tumetoa ushauri hapa; labda wale wajumbe wateuliwe kwa muda tofautitofauti, si wako wanne, leo teua wanne, halafu mwakani teua wanne, ili kwamba hawa wanne wakimaliza wanne wabaki wana-save. Au tuletewe sheria tubadilishe, tuseme kwamba bodi hata kama ikimaliza muda wake kwa mujibu wa utaratibu, kama haijatumbuliwa basi iendelee kufanya kazi mpaka pale ambapo bodi nyingine itakapopatikana na si kuacha tu Katibu Mkuu pale eti ameshikilia. Kuna bodi zingine unashangaa wamemaliza vizuri unakaa hata mwaka baadaye wanarudishwa walewale, sasa maana yake nini?

Mheshimiwa Spika, mimi nadhani tuweke utaratibu, watu kama huwataki watumbue waondoke, lakini kama hujawatumbua muda wao umeisha hujaleta wengine wapya, Serikali iwaache waendee kukaa kama bodi ili waweze kuteua watu wengine.

Mheshimiwa Spika, nataka niguse kidogo kuhusu Bodi ya Mikopo. Pale Bodi ya Mikopo, mimi juzi nilikuwa napitia ripoti ya CAG, nikagundua hata walivyokuwa wanamgomea Waziri wao kwa kweli sijashangaa. Ukipitia ile ripoti ya CAG vizuri huwezi kushangaa kwa nini Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ilikuwa inamgomea Waziri wake, kwamba ile kamati yake hawataki kuipa ushirikiano, yaani huwezi ukashangaa.

Mheshimiwa Spika, watakuja kusema wenyewe kwa sababu umewaita. Lakini madudu yaliyoko kwenye ripoti ya CAG kuhusu Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ni jambo serious na ambalo mnahitaji kufanya hatua za haraka sana; na ndiyo maana hawataki kuchunguzwa maana ukiwachunguza utaona madudu yao. Lakini CAG ameshatusaidia kuyaonyesha yatima hawapati mikopo, maskini hawapati mikopo, wanatoa hela excess ambazo hawatakiwi kutoa, zaidi ya nilioni tano. Sasa unataka uambiwe na nani kwamba hawa watu hawafai?

Mheshimiwa Spika, mimi niseme, tunao utajiri mkubwa sana kupitia mashirika haya, hayawezi kuwa operated kama mashirika ya Private Sector lakini yapo mambo ambayo tunaweza tukakopa kule tukayaleta kwetu, tukabadilisha sheria zetu kama ndicho kikwazo ili tuhakikishe tunaweza kwenda kwa speed ambayo Mheshimiwa Rais anaitaka. Mheshimiwa Rais anasema kazi iendelee lakini yako mashirika ambayo hayaendani na kauli mbiu ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja nashukuru sana sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nishukuru kwa kunipa nafasi hii angalau niweze kuchangia kidogo kwenye Hotuba ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, niungane na wenzangu kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, lakini pia na Waziri Mkuu pamoja na Baraza lake la Mawaziri kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea nayo na kasi ya hapa kazi tu ambayo sifa zake zimetamalaki Tanzania nzima lakini pia na nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi nilishukuru sana kuona kwamba barabara ya Kidahwe - Nyakanazi imewekwa kwenye kipaumbele, Malagalasi hydropower ipo na Kiwanda cha Sukari - Kigoma Sugar nacho pia kimepewa kipaumbele. Najua haya yatakuwa ni chachu ya maendeleo katika Mkoa wetu wa Kigoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia suala la umeme wa REA. Naomba Waziri mwenye dhamana husika, Mzee wangu Mheshimiwa Profesa Muhongo, lakini pia Naibu Waziri wake, suala la umeme wa REA katika Jimbo langu la Kasulu Vijijini bado utekelezaji wake siyo mzuri, ni wa kusuasua. Nashukuru sana Naibu Waziri alifika Jimboni kwangu pale tukaweka mikakati mizuri lakini napenda kumkumbusha tu kwamba, bado utekelezaji siyo mzuri na aweze kusukuma kuhakikisha kwamba umeme wa REA unafika kwenye Jimbo langu la Kasulu Vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa mapato, nipende kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa namna ambavyo imeendelea kuongeza kukusanya mapato kila mwezi. Napenda kuwakumbusha kwamba mpakani kule bado zipo fedha zinapotea. Jimbo langu limepakana na nchi ya Burundi, kule wako watu ambao bado wanaingia pasipo kutozwa ushuru formally. Pia fedha zingine zinaishia kwa wajanja wachache ambao ni Maafisa. Kwa hiyo, ni bora sasa, Wizara husika ikaenda kuweka pale utaratibu wa namna ya kukusanya fedha zile ambazo zitakuja kusaidia Halmashauri yetu lakini pia na nchi nzima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimdokeze Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mzee wangu Mheshimiwa Simbachawene kwamba pale Kasulu bado kuna majipu, nakuomba sana utue mahali pale. Ripoti ya CAG mwaka jana ilionyesha upotevu wa shilingi bilioni 5.9, lakini mpaka leo hakuna kitu ambacho kimefanyika kushughulikia watu ambao walihusika na upotevu ule. Watumishi walikuwepo lakini pia na viongozi wa halmashauri walikuwepo. Kwa hiyo, ni vyema Mheshimiwa ukatua pale kwa ajili ya kushughulikia watu hawa ili fedha zile ziweze kuja kuwasaidia wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kilimo. Mheshimiwa Mwigulu, wananchi wanakusubiri sana Jimbo la Kasulu Vijijini uende ukamalize tatizo au mgogoro wa pori la Kagerankanda. Wananchi kwa muda mrefu sana hawana maeneo ya kutosha kwa ajili ya kilimo kwa sababu tu ya uwepo wa hifadhi ya pori la Kagerankanda ambalo kimsingi ukiangalia uhitaji wake sio mkubwa. Nadhani mipaka ile ilichorwa zamani wakati ambapo uhitaji wa ardhi haukuwa mkubwa. Kwa sasa kimsingi hatuwezi kuendelea kufuga miti ile ilhali watu wanakufa na njaa. Kwa hiyo, nikusihi sana Mheshimiwa Waziri uweze kufika pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Bunge lililopita Mheshimiwa Waziri ulisema kwamba, Wabunge tuje hapa tuseme ni lini tunahitaji mbolea za ruzuku ziweze kufika Jimboni kwetu. Naomba niseme kwamba Jimbo la Kasulu Vijijini tunahitaji tupokee mbolea ya ruzuku mwezi wa nane kila mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, nipende kusisitiza tu kwamba, Watanzania wa Jimbo la Kasulu Vijijini wanayo imani kubwa sana na Serikali ya Awamu ya Tano na wana imani kubwa sana na kasi ambayo inakwenda nayo. Niwatie nguvu sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, hizi mbwembwe ambazo unaziona hapa, watu kugomea kuchangia na kususia vikao vya Bunge, hizi sarakasi tu wanajaribu kupanda kichuguu wakati mvua imenyesha, ni suala la kisikitisha sana. Nadhani hata Watanzania wanashuhudia nini kinatokea. Watu ambao waliwachagua kwa ajili ya kuja kimsingi kuwasilisha matatizo yao na kuyashughulikia wakisusia vikao mahsusi ambavyo vingeenda kutatua matatizo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niwashauri ndugu zangu Wapinzani lakini pia na uongozi wa Bunge hebu tumshauri Mheshimiwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni akae chini atafakari aone kama nafasi ya kuwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni bado inamfaa, ajipime vizuri. Kwa sababu ukiangalia namna ambavyo anaendesha kambi hii ni kinyume kabisa na matarajio ya Watanzania ambao wanahitaji maendeleo kwa nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wa Upinzani napenda kuwashauri kitu kimoja, nimesikia wakiitwa majina mengi sana ambayo mengine siyo mazuri kuyataja, lakini suala la kuja kujipanga kugomea mipango madhubuti ya kwenda kutatua matatizo ya wananchi, kujipanga kuchafua Serikali ambayo inakwenda kwa kasi ya ajabu, kujipanga kukwamisha maendeleo kwa namna yoyote siyo tabia ya kibinadamu ni tabia ya kinyama kabisa ambayo inafaa kulaaniwa na watu wote wanaopenda maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua wako watu ambao wakati mwingine wanalazimishwa kufikiria kinyume na vile ambavyo wanaamini kwa sababu tu labda kiongozi amesema, wanalazimika kufuata vile ambavyo wameelekezwa. Tabia hii wako wanyama ambao kiongozi akitangulia bila kujua anaelekea wapi, anaelekea shimoni, anaelekea mtoni au kiongozi wa wanyama wale anaelekea kwenye miiba, anaelekea kuliwa na mamba, wao huunga mkono na kumfuata nyuma, wanyama hawa wanaitwa nyumbu. (Makofi)
KUHUSU UTARATIBU
MWENYEKITI: Kuhusu utaratibu.....
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru tu sana na nisingependa muongeaji anifanye nikaenda mbali zaidi kwa sababu kama ni kuminya demokrasia wao ni vinara na hayo yamejidhihirisha wazi, hata kupitia kwenye Kamati za LAAC na PAC ambapo wajumbe wako wa Upinzani na wa CCM lakini…
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na nina imani muda wangu umeulinda vizuri maana wanajaribu kunitoa kwenye mstari ili nisiseme kile ambacho nataka kukisema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme tu kwamba hapa ni Bungeni na kila mtu kaja kwa kura ambazo amepewa na wananchi na kila mtu anao uhuru wa kusema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikumbushe tu jambo moja kwamba wako watu ambao wakati mwingine wanajaribu kukuondoa kwenye kile ambacho unahitaji kuzungumza, labda niachane nayo hayo. Tuko hapa mbali na kuzungumza namna ya kuleta maendeleo ya kiuchumi ya nchi yetu lakini pia lazima tuweke sawa ili kuhakikisha kwamba tunalinda misingi ya demokrasia na kuikuza vizuri na hatimaye nchi yetu iwe katika nafasi nzuri sana katika nyanja ya demokrasia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi nimeyazungumza hapa lakini itoshe kusema kwamba naunga mkono hoja vizuri kwa asilimia 100 na Serikali ya Awamu ya Tano iendelee kuchapa kazi vizuri na wana CHADEMA wakubali wajumbe wa PAC na LAAC watoke CUF bila kinyongo chochote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kukushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adimu ya mimi kuweza kuchangia kwenye hotuba ya Waziri wa Katiba na Sheria, lakini pia na hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipende kueleza masikitiko yangu kwa hali ambayo imejitokeza jioni ya leo. Ama kweli hii imedhihirisha kwamba mkuki kwa nguruwe lakini kwa binadamu ni mchungu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye hoja, kwanza napenda kumshukuru Mzee wangu Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe kwa kutuonyesha umahiri wake leo tena kwa kupitia hotuba yake ambayo ameitoa hapa. Napenda kulikumbusha Bunge hili kwamba umahiri wa Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe haujaanza leo, huyu ndiye aliyeongoza Kamati ambayo ilimuondoa madarakani fisadi papa namba moja Ndugu Edward Ngoyai Lowassa. Mzee Mwakyembe tunakushukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe yako mambo machache ya kukushauri tu mzee wangu. Suala la kwanza ni Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini ya 2006…
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Kifungu 32(1), nanukuu, kinasema; ―Mfanyakazi atakuwa na haki ya likizo ya ugonjwa angalau siku 126 kwa kila mzunguko wa likizo.‖
Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili limeleta utata wakati mwingine kwa sababu wako wagonjwa ambao wameugua zaidi ya muda huu. Naomba sana kipengele hiki kiweze kurekebishwa ili watu wapate nafasi ya kuweza kutibiwa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni la wafanyakazi wa migodini. Watu hawa wamekuwa wakifanya kazi ngumu na wakati mwingine kulingana na mazingira duni ya migodini wamekuwa wakipata shida au matatizo ya kiafya na mara baada ya kupata matatizo ya kiafya huwa wanaachwa na waajiri wao na hatimaye wanakuwa maskini wakubwa sana. Kwa hiyo, ningeomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kwenye majumuisho hili nalo alizungumzie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimejikita tena kwenye hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni…
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia ukurasa wa 11, Mheshimiwa Tundu Lissu anasema kunyamazisha upinzani na kukaribisha udikteta. Labda niwakumbushe watu hawa kwamba upinzani umejiua wenyewe yaani wamejikaanga kwa mafuta yao wenyewe. Moja, wamejikaanga kwa unafiki wao uliopitiliza, nitasema hapa ambao hasa umeongozwa na huyu huyu ambaye ni Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria.
KUHUSU UTARATIBU...
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme tu kwamba kwa taarifa zilizozagaa na ambazo kila Mtanzania anazifahamu...
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba wagonjwa wa namna hii kwao wako wengi, mbona Mheshimiwa Mnyika yuko Muhimbili naye anatibiwa hivyo hivyo tu.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kwa mujibu wa Kanuni nifute kauli hiyo ya Mirembe na naomba kuendelea na unilindie muda wangu. (Makofi)
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nilisema hayo kwamba nimejiridhisha na kauli hizo za mtaani kwa sababu moja ya unafiki…
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mtu huyu amekuwa ni mnafiki namba moja katika nchi hii. Nitathibitisha unafiki na uongo wake.
Kwanza wakati anachangia hapa amesema eti anashangaa kwa nini Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania hajastaafu wakati aliosoma nao wamestaafu, anashindwa kujua kwamba siyo kila unayesoma naye umri wake ni sawa.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Amesema aliosoma nao. Wakati mimi nasoma nimesoma na watu ambao wana umri wa baba yangu lakini mtu huyu ni msomi na anajua mambo yote haya anaamua kupotosha Taifa kupitia chombo kitakatifu cha Bunge kwa makusudi kabisa. Ndiyo maana nasema unafiki huu unanirejesha kwenye hizi rumors ambazo nimesikia mtaani.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hilo nimeshafuta na mimi naendelea na mchango wangu. Sasa kama unaniambia kwamba niache kuchangia kwa kumzungumzia mtu huyu…
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Hapa nafanya hivyo ili kuweka record clear, kwa namna ambavyo amepotosha Bunge, kwa namna ambavyo …
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba unilindie muda wangu. Wewe unataka nini?
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilindwe kwa mujibu wa Kanuni. Nimekuja hapa kwa mujibu wa Kanuni.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri. Afya ni msingi wa maisha ya binadamu awaye yote kwa vile kuwa na afya mgogoro ni chanzo cha kufilisika kwa shughuli zote za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya kabisa Wilaya yetu ya Mbogwe mwaka huu wa fedha Halmashauri yetu iliweka katika bajeti yake jumla ya shilingi bilioni 1.5, hata hivyo kutokana na ukomo wa bajeti fedha hizo zikaondolewa kwenye bajeti. Naishauri Serikali yetu ione umuhimu wa kusaidia ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Mbogwe. Tuna taabu Mbogwe, sikieni kilio chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kutujengea theatre mbili katika vituo vya afya vya Masumbwe na Mbogwe ambapo Shirika la Umoja wa Mataifa la UNFPA kwa kushirikiana na Wizara ya Afya na kuvipatia vituo hivi vya afya ambulance mbili, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kituo cha afya cha Mbogwe bado hakijafunguliwa rasmi kwa vile vifaa havijakamilika katika theater licha ya kwamba kweli gari la wagonjwa la UNFPA lipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbogwe tuna uhaba mkubwa wa watumishi katika Idara ya Afya kwenye vituo vya afya na zahanati, naiomba Serikali ilione jambo hili na itupatie watumishi wa kutosha Wilayani kwetu.

Mhesimiwa Mwenyekiti, aidha naiomba Serikali itusaidie kukamilisha ujenzi wa vituo vya afya vya Ilolangula Ikunguigazi, Ikobe, Nhomolwa, pamoja na ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Mbogwe ili kuboresha huduma za afya Wilayani Mbogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Geita ni mpya tunahitaji hospitali ya rufaa yenye uwezo wa kuhudumia wananchi wilayani wanapopata rufaa. Ujenzi wa hospitali ya rufaa utakuwa ukombozi kwa wananchi wa Mkoa mpya wa Geita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru, ahsante kwanza awali ya yote nipende kupongeza na niseme naunga mkono hoja ya hotuba ya Waziri Mkuu.

Pia napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kutupa uhai huu, Waziri Mkuu hotuba yako ni nzuri sana. Imeeleza ni namna gani ambavyo Serikali imejipanga na kujipambanua lakini namna gani ambavyo imekuwa ikitekeleza Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite kwanza na yale mambo ambayo yapo kwenye Jimbo langu. Nipende kushukuru Serikali, nipende kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa hela ambazo ametupa jimbo la Kasulu Vijijini shilingi milioni 500 kwa ajili ya ukarabati wa kituo cha afya pale Nyakitonto lakini pia shilingi milioni 200 kwa ajili ya ukarabati wa kituo cha afya pale Hospitali ya Muyowozi lakini nipende kushukuru Serikali pia kupitia Waziri wa Afya kwa namna ambavyo ananipa ushirikiano pamoja na TAMISEMI kwenda kuanzia Hospitali ya Wilaya pale Muzye, pale mkandarasi atamaliza kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la viwanda nipende kumwomba Mheshimiwa Mwijage na Serikali kwa ujumla kwamba kuna mwekezaji alikuja kwetu pale Kigoma Sugar kwenye Jimbo langu. Mwekezaji yule alipewa ardhi ili aweze kufanya kilimo cha miwa na kuanzisha kiwanda, lakini ameshindwa kufanya hivyo na ameenda kinyume na mkataba. Sasa tunaomba Serikali iweze kumnyang’a mtu huyu eneo lile na hatimaye waweze kuwavutia uwekezaji kwa watu wengine ili kwamba watu wengine waweze kujitokeza na kufanya kilimo cha miwa na hatimaye kiwanda cha sukari tuweze kuwanufaisha watu wa Kasulu Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Maliasili na Utalii, tarehe 20 Julai kama sikosei Mheshimiwa Rais alikuja Wilaya ya Kasulu, pomaja na mambo mengine ambayo alisema aliruhusu wananchi waendelee kulima sehemu ya kipande cha msitu wa Makere kusini yaani Kagerankanda na alifanya hivyo kutokana na mateso makubwa ambayo wananchi walikuwa wakiyapata kwa kupigwa na watu wa Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha ajabu wako watu ambao sijajua kiburi wanakitoa wapi, wanaendelea kuwanyanyasa watu ambao wanaenda kulima Kagerankanda, hii haikubaliki ni kinyume cha maelekezo ya Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, niombe chonde chonde Mheshimiwa Kigwangalla umenipa ushirikiano katika hili, tulimalize hili wananchi waendelee kulima vizuri na hatimaye waweza kufaidi kauli ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Waziri Mkuu chapa kazi, yasema nguvu ya mamba iko kwenye maji; na maji yako wewe ni sisi tupo, tuko nyuma yako tunaona kazi kubwa ambayo wewe pamoja na Mheshimiwa Rais mnaifanya kwa ajili ya Watanzania leo haya mambo mengine makelele hayo tuachane nayo nawaambia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwepo Bungeni hapa kwa muda wa miaka kama miwili na kidogo. Moja ya kitu ambacho nimegundua humu Bungeni ni kwamba tunayo macho mawili ya kibinadamu. Liko jicho ambalo ni zima lenye afya lakini liko jicho ambalo lina chongo humu ndani. Nasema hivyo kwa sababu gani, haiwezekani watu tunawambia Serikali inajenga na imeanza ujenzi wa Standard Gauge Railway kutoka Dar es Salaam na Mkandarasi amepatikana na ujenzi umeanza lakini watu wanabeza wanaona kama ni reli ya udongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti,haiwezekani tuwaambie watu kwamba tunanunua ndege na ndege zimekwishafika tatu zimeonekana, lakini watu wanazibeza wanaona kama ni parachute sio ndege. Tunawaambia watu kwamba hawa watu huyu kwamba hao viongozi wenu wana matatizo, wanafanya makosa wanaenda kinyume na utaratibu na wanapaswa washughulikiwe kama wahalifu wengine wao wanaona hapana wanaonewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nipende kusema kitu kimoja, ifike pahala tujitahidi sana kutenganisha kati ya kazi ya vyombo na Mheshimiwa Rais maana mtu anafanya makosa, anaenda kinyume na utaratibu, anavunja sheria halafu akianza kushughulikiwa, unakuta watu wanasema kwamba anashughulikiwa na Mheshimiwa Rais nani kasema? Nani kasema, hii ni nchi ambayo inaongozwa kwa mujibu wa sheria mtu yeyote anapokuwa amefanya makosa inapaswa ashughulikiwe kama mhalifu mwingine. Haya maneno ya watu kukimbia kwenda wapi kwenda kwa mabwana zao kutafuta sijui…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha muda wa Mzungumzaji)
TAARIFA YA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE KUHUSU SHAURI LA KUDHARAU NA KUDHALILISHA BUNGE LINALOMKABILI NDUGU PROF. MUSSA ASSAD, MDHIBITI NA MKAGUZI MKUU WA HESABU ZA SERIKALI
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru kwa nafasi hii nami kuchangia hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nianze kwa kunukuu maneno ya Mheshimiwa Mwalimu Nyerere Baba wa Taifa letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliwahi kusema kwamba, “uhuru bila nidhamu ni wazimu.” Nadhani hata kaka yangu Mheshimiwa Mbowe analifahamu hilo kwamba tuna uhuru lakini lazima uhuru uwe na mipaka. Ndiyo maana hata wakati ule akina Mheshimiwa Kubenea walipoona kwamba wana uhuru usio na nidhamu na kuanza kuikosoa Kamati Kuu ya CHADEMA, waliitwa kwenye Kamati Kuu na wakapewa onyo kali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, japo taarifa ya CHADEMA ilionesha kwamba…

WABUNGE FULANI: Walisamehewa.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Taarifa ya CHADEMA ilionesha kwamba walikiri kosa...

WABUNGE FULANI: Walisamehewa.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Vuma naomba utoke kwenye kiti chako uende upande huu, tafuta kiti pale sehemu ya kukaa, ili upate nafasi ya kuchangia vizuri kwa sababu kuna watu humu ndani huwa wanaamua kufanya fujo kama wao jambo lao haliendi sawasawa. Mheshimiwa Vuma. (Makofi)

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze upya. Nasema, nimeanza kwa kunukuu kauli ya Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere. Aliwahi kusema, “uhuru bila nidhamu ni wazimu.” Maana yake ni kwamba hakuna uhuru usio na mipaka. Nikaenda mbele kwa kusema, hata kaka yangu Mheshimiwa Mbowe analifahamu hilo, ndiyo maana wakati ule ambapo akina Mheshimiwa Kubenea na Mheshimiwa Mzee Komu walipodhani wana uhuru usio na mipaka wakakaa kuikosoa Kamati Kuu ya CHADEMA Kamati Kuu iliwaita na kuwapa onyo kali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa iliyotoka kwa Umma ya CHADEMA ilionesha wale watu walikuwa waungwana wakakiri makosa, lakini bado walipewa jukumu la kwenda mbele ya jamii na kuomba radhi wana-CHADEMA wote. Sasa kama CAG angekuja hapa akakiri kosa akaomba radhi, labda tungefikiria. Hajawa muungwana kama walivyokuwa akina Mheshimiwa Kubenea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niseme, kazi ya Bunge mnavyofahamu na Waheshimiwa Wabunge tukubaliane jambo moja, tunao wajibu wa kulinda madaraka ya Bunge kwa wivu. Haiwezekani Bunge lije lichafuliwe, halafu wewe Mheshimiwa Mbunge ubaki uko salama. (Makofi)

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa najua kazi ya Bunge ni kutunga sheria, kuisimamia Serikali na kuwakilisha wananchi. Kwenye kutunga sheria tumeona Bunge hili linatunga sheria nzuri kwa ajili ya wananchi. Mwaka 2018 tumetunga sheria ya kurekebisha Sheria ya Madini ambayo tumeona imeongeza mapato kwa Taifa letu; Bunge hili la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama haitoshi, kwenye kusimamia Serikali, mimi niko Kamati ya PIC, tunasimamia mashirika ya Umma zaidi ya mashirika 200 na tumeona mwaka 2018 kwa sababu tumekuwa tukiwapa maelekezo mazito kwa mara ya kwanza mashirika ya Umma yameanza kutoa gawio kubwa. Mwaka 2018 walitoa zaidi ya shilingi bilioni 700 na tunategemea mwaka huu watatoa zaidi ya shilingi trilioni moja. Hiyo ni kazi ya Bunge kusimamia Serikali kufanya kazi. Tunawakilisha vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hizo hizo na miongozo ambayo Bunge inatunga na kutoa kwa Serikali ndio imesababisha nchi inatawalika, nchi hii imekuwa nzuri. Juzi kumetoka report ya Global Peace Index ambayo inaonesha Tanzania kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki ni nchi ya kwanza kwa kuwa na amani, lakini ni ya saba Afrika na ya 51 duniani. Sasa anatoka mtu anakuja anasema Bunge ni dhaifu, anapata wapi mamlaka hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naunga mkono hoja. CAG ametukosea adabu, ametukosea heshima, nami naunga mkono hoja ya Kamati kwamba hatuko tayari kufanya naye kazi. Tunahitaji mtu mwingine ambaye tutakuwa tunaongea mamoja, twende pamoja kusaidia Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia kwenye bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Mchango wangu utajikita sana kwenye shukurani, maombi, pia na ushauri. Nitaanza na la mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kushauri kwanza kwenye suala la vibali vya ajira. Nchi yetu hii tunavyojua ni kwamba ina soko dogo sana la ajira. Ajira ni chache lakini tunao vijana wengi ambao hawana ajira. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Jenista na Ofisi yake kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kwenye kudhibiti otoaji holela wa vibali vya ajira. Maana hapo katikati vibali hivi vimekuwa vinatolewa kama njugu, sasa sisi kama Taifa tuna uhitaji mkubwa wa ajita kwa sababu kuna vina wengi ambao wako mtaani. Nashangaa kuna watu ambao wanakuja hapa Bungeni kutetea kwamba Serikali izidi kumwaga vibali vya ajira hii kwa wawekezaji mbalimbali. Jambo la ajabu kabisa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kwa sababu tuna vijana wengi ambao wako mtaani, Mheshimiwa Jenista na ofisi yake waendelee kuminya. Nimpongeze Kamishna wa Ajira, waendelee kuminya, wasitoe vibali hivi kwa wageni ili wananchi wa Tanzania, vijana wengi ambao wako mtaani ambao hawana ajira, waendelee kupata kazi hizi. Hili ni jambo la kwanza. Niseme, kwa sababu tunajua kuna shida, tatizo kubwa la ajira nchini, mimi nitoe ushauri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, kwamba iundwe Task Force, yaani Kikosi Kazi, chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ambacho kitajumuisha wasomi, wajasiriamali na wadau mbalimbali ili kuweza kujadili tatizo hili la ajira nchini na hatimaye waweze kutoa ushauri mzuri kwa Serikali yetu pendwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua, Serikali inaendelea na juhudi zake za kuendelea kutoa ajira kwa maelfu…

MHE. ALLY SALEH ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Vuma, taarifa.

MHE. ALLY SALEH ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa taarifa msemaji, hoja iliyopo hapa ni ile sheria inayosema kwamba, mwekezaji ana fursa ya kuleta watu watano wa mwanzo, automatic bila hata akileta mtu wa aina gani, wale ambao watamlindia mali yake. Kwa hiyo, hawa kwa nini wanasumbuliwa ndiyo hoja, napenda kumpa taarifa hiyo, wakati wameshatajwa kwenye sheria.

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Augustine taarifa hiyo unasemaje?

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei, kwa sababu Kamishna wa Ardhi anaifahamu vizuri kabisa Sera na Sheria yetu, amekuwa anawanyima vibali watu ambao hawana sifa za kupata vibali vya kuajiriwa, kabisa, kwa sababu nina watu ambao nimeshuhudia kwa macho yangu, wenye vigezo, wanapata vibali. Kwa hiyo, wale ambao wananyimwa ni wale ambao hawana vigezo na nashauri Kamishna wa Ardhi aendelee kukaza buti, kwa sababu kuna vijana, kuna wadogo zetu, kuna watoto wengi ambao wako mtaani ambao hawana kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri Ofisi ya Mheshimiwa Kairuki, Uwekezaji, kwamba niko Kamati ya PIC tuna Mashirika mengi ya Serikali, tuna mashirika mengi ya Serikali ambayo yana fedha nyingi sana. Badala ya mashirika haya kwenda kujikita kuwekeza kwenye ujenzi wa majengo ya nyumba za kuishi, sijui za biashara, nashauri, washauriwe watu hawa waende kuwekeza kwenye sekta ambazo zitawagusa Watanzania walio wengi sana, hususan kwenye kujenga viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nitoe ushauri mmoja, kwamba katika Awamu hii ya Tano, ambayo tunajua kwamba ni Serikali ya Viwanda, ningeweza kushauri kwamba, Mheshimiwa Waziri akae na Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii, hasa NSSF, PSSPF,waweze kukaa pamoja na kutafuta wadau mbalimbali wengine ambao wataunganisha nguvu pamoja, tupate kiwanda kikubwa cha mbolea katika nchi hii ili tuweze kuondokana na tatizo la kuagiza mbolea kila mwaka kutoka nje ya nchi, ushauri huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri kwenye suala pia la internship, vijana wengi ambao wanamaliza vyuoni wanakaa mtaani na wakati mwingine wanakosa ajira katika sehemu mbalimbali kwa sababu ya ukosefu wa uzoefu. Sasa nashauri, Serikali iwe na mkakati wa kutoa internship kwa vijana ambao wanamaliza vyuoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua huwa tuna utaratibu, tuna mipango kwamba baada ya mwaka mmoja tunaajiri watu kadhaa, baada ya miaka mitano tutaajiri vijana kadhaa. Sasa ushauri wangu ni kwamba, vijana wanapokuwa wamemaliza vyuo vikuu, basi tuwe na utaratibu kabla haujafika wakati wa kuwaajiri, tuwachukue tuwaweke sehemu mbalimbali katika ofisi za Serikali, kwenye mashule, mahospitali na sehemu nyingine, waende wakajifunze kuchapa kazi ili wasiwe tu na elimu bali pia wawe na uzoefu wa kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wengi wako tayari kujitolea, kwa sababu wanajua kwamba kwenye kujitolea wanapata uzoefu na hatimaye wanakuwa na nafasi ya kupata kazi hata kwenye sekta binafsi kwa sababu wanakuwa na uzoefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maombi, Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu, tumepanga, kwa sababu Makao Makuu ya Halmashauri yako kwenye Halmashauri ya Kasulu Mji, kwa mzee wangu Nsanzugwako pale. Naomba Serikalini, kwamba eneo la kujenga Makao Makuu ya Halmashauri, tunalo tayari, pale Kata ya Nyamnyusi, kwa hiyo, niombe fedha kwa ajili ya ujenzi wa halmashauri ili kwamba tuweze kutoka Kasulu Mjini, twende sehemu yetu kwa maana ya kuwafuata wananchi na kuwapelekea huduma zaidi karibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Chuo cha Ufundi cha Nyamidahu, hiki chuo tumejengewa na World Vision, wamejenga chuo kizuri kina mabweni, kina madarasa, kina furnitures, lakini sasa hakina vyoo, hakina umeme na miundombinu midogomidogo. Kwa hiyo, niombe Serikali kwamba ikichukue chuo hiki, ikimalizie, kwa sababu kina zaidi ya miaka mitatu toka kikamilike ili kiweze kuanza kutumika kuwanufaisha wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi lingine, kwa sababu tunaendelea na miradi ya umeme miwili, kwenye Jimbo la Kasulu Vijijini na Mkoa wa Kigoma kwa ujumla, tunaendelea na REA, lakini na ujio wa Gridi ya Taifa. Najua kwenye gridi ya Taifa, evaluation imefikia asilimia 90, na mwezi wa Sita kwa maelezo niliyonayo, kwamba watakuwa wamemaliza tayari evaluation. Wananchi wa Mkoa wa Kigoma wamesubiri kwa muda mrefu sana ujio wa umeme wa gridi ya Taifa, kwa hiyo, niombe chonde chonde evaluation itakapokamilika, kwenye bajeti hii ambayo tunaipitisha muda si mrefu, ya mwezi wa Sita, basi wananchi wa Kigoma tuhakikishe kwenye bajeti hii wanapata umeme wa gridi ya Taifa kwa sababu tumesubiri muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipende kuomba pia, tumepata vibali vya miradi ya maji, miradi ya Nyamnyusi, Titye na Lalambe kule, zaidi ya bilioni sita, tumepata vibali vya kutangaza tenda hizi. Niombe tutakapopata mkandarasi kusiwepo na ucheleweshwaji wa fedha kutoka Serikalini kwa ajili ya mkandarasi huyu ili kuhakikisha kwamba mradi unakamilika kwa wakati na wananchi waweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishukuru Serikali, kuna vitu vingi sana ambavyo imefanya kwenye Jimbo la Kasulu Vijijini. Tumepata milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya cha Nyamidaho, tumepata milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya cha Rusesa Uboreshaji, tumepata milioni 500 ujenzi wa kituo cha afya cha Nyakitonto, tumepata bilioni moja na milioni mia tano kwa ajili ya ujenzi ya hospitali mpya ya Wilaya kwenye Kata ya Nyamnyusi. Napenda kuishukuru sana Serikali, kwa kweli kazi kubwa imefanyika, kazi kubwa mno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye elimu, juzi tumepata fedha milioni mia tatu kwa ajili ya ujenzi wa mabweni na kupanua Sekondari ya Kasangezi. Tumepata fedha tumemalizia shule ya Asante Nyerere, imeanza tumesajili, tumepata fedha tumemalizia shule ya Sekondari Kitanga imeanza tayari, lakini pia tumepeleka milioni 48 kwenye shule ya msingi Shunga. Kwa kweli kazi kubwa inafanyika, na niwaambieni, mwaka 2020, Magufuli Kasulu yeye aje apunge mkono tu atashinda. (Makofi/Kicheko/Vigelegele)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Vuma ahsante sana.

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ambayo nimeipata jioni ya leo kuchangia kwenye bajeti hii. Nipende kwanza kuipongeza Serikali, kwanza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli na nimtakie kila la kheri kwenye ziara yake aliyopo nchini Namibia arudi salama, tunamuombea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kumpongeza pia Waziri na Naibu Waziri na Timu nzima ya Wizara ya Nishati kwa kazi kubwa ambayo wanafanya kuhakikisha kwamba wanatuletea maendeleo katika sekta hii. Najua mkandarasi wa kule Kigoma na Katavi wameanza utekelezaji wa mradi ule late kidogo, lakini naamini kwamba kama Serikali ambavyo imekuwa ikielekeza wakandarasi kumaliza miradi kabla ya wakati nina imani kwamba mkandarasi ambaye anafanya kazi Mkoa wa Kigoma naye atamaliza kwa wakati na kuhakikisha kwamba Kata zangu za Nyachenda, Bugaga, Buzye, Kasangezi, Lusesa, Kalela, Lungompya na nyingine zinapata umeme kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende pia kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa na maamuzi magumu ambayo walifanya kwenye mradi wa Rufiji Hydro Power. Naomba niseme kitu kimoja, ndugu zangu nimekaa hapa nikiwa nasikiliza michango ya watu tangu mwaka jana na mwaka huu nimeona, hasa ndugu zetu wa upande wa pili. Niseme Rais wa Awamu ya Nne aliwahi kusema kwamba akili za kuambiwa changanya na za kwako, akimaanisha usiamini kila unachoambiwa. Sasa ndugu zangu kwa sababu mabeberu wamekuwa wanakataa mradi huu ambao ni very potential kwa Taifa letu, msiingie kwenye mgogoro wa kuwasapoti ili hali mnajitoa ufahamu kwa faida za mradi huu wa Rufiji Hydro Power. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niseme tu kwa faida ya Watanzania, Mradi huu wa Rufiji Hydropower una faida nyingi sana kwa Watanzania na Taifa kwa ujumla. Faida ya kwanza kabisa tunaenda kupata umeme ambao tunaupata kwa bei ndogo kuliko umeme wa chanzo chochote katika nchi hii, namba moja kabisa. Tunaenda kupata umeme mwingi; kwa study iliyopo kwamba katika nchi yetu ya Tanzania hakuna chanzo chochote cha nishati ya umeme ambacho kinaweza kikatoa nishati ya bei ndogo lakini kwa wingi kama chanzo cha maji. Kwa hiyo uamuzi wa Serikali kujikita kwenye miradi ya kuzalisha umeme wa maji ni uamuzi sahihi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, faida ya pili, mradi ule ukiusoma vizuri utaona kwamba kutakuwa na miradi ya uvuvi pia. Wanavyojenga lile bwawa kutakuwa kuna potential watu kufanya shughuli za uvuvi ambayo ni shughuli ya kiuchumi ikayoweza kuwasaidia wananchi ambao watafanya shughuli hiyo. Sababu ya pili au faida ya pili, tunategemea mradi ule kutakuwa na umwagiliaji, watu wanafanya kilimo cha mpunga na miwa na study inaonesha kwamba mpunga au mchele utakaotoka kule kwenye bonde lile utaweza kulisha Afrika Mashariki na Kati, sasa wanakataa nini kwenye mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye sababu nyingine, ule mradi kwa sababu ni wa kipekee nawahakikishieni ule mradi utakuwa ni kivutio cha utalii Afrika Mashariki. Wako watu ambao wakija Tanzania watataka kwenda kuona kule Rufiji Hydro Power namna ambavyo ilivyo na kujifunza. Pia huu mradi naamini, nitofautiane na wengi ambao wanaamini kwamba huu mradi unaenda kuharibu mazingira, niseme huu mradi unaenda kutunza mazingira kwa sababu gani, wananchi wengi vijijini kule wanatumia nishati ya kuni kwa ajili ya kuleta mwanga lakini pia na kupika. Kama haitoshi wanatumia vibatari kwa ajili ya nishati ya mwanga. Sasa umeme unapokuwa umeenda tunaamini kwamba matumizi ya kuni yatapungua lakini na matumizi ya vibatari yatapungua. Huo utakuwa ni utunzaji wa mazingira kupitia mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme huu mradi mimi naufananisha na three gorges ya China, huu mradi ulianzishwa na Rais wa kwanza wa China ambaye alikuwa anaitwa Sun Yat-Sen. Huu ni kama vile mradi wetu huu ilivyokuwa wazo la Mwalimu Nyerere vilevile na ulibuniwa zaidi kabla ya mwaka 1980, huu wa three gorges. Sasa kwa sababu ya figisu figisu kama ambazo tunasema hapa kwetu Tanzania, huu mradi ulianza kutekelezwa kuanzia miaka 1990.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutekelezwa kwa mradi huu kulitokea baada ya Bunge la China kupiga kura kwamba kama nchi inahitaji mradi huu au haihitaji. Walivyopiga kura theluthi mbili ya Wabunge wa China wakakubali kwamba mradi huu wanautaka kama Taifa. Sasa niseme sisi wameleta bajeti hapa Wizara mwaka jana kuomba bilioni 700 kwa ajili ya mradi huu, sisi Wabunge wa CCM nadhani na wa CUF ambao ni zaidi ya robo tatu, zaidi ya idadi ya ile ya Wachina ambao ilipisha mradi ule tulisema tunahitaji Mradi wa Rufiji Hydro Power. Kwa hiyo niwaambie Serikali, hili jambo lina baraka ya Bunge na ndiyo maana mwaka jana tuliwapa bilioni 700 na nina imani hela zimefanya kazi ipasavyo na tunawaunga mkono katika hilo.

Mheshimiwa Spika, na niseme, lazima Serikali muwe imara, msiyumbishwe na miluzi. Kule China wakati wanajenga mradi huu kuna watu baada ya kupiga kura Bungeni, ilitolewa amri ya Serikali kwamba hairuhusiwi mtu yeyote kupinga mradi huu na mtu aliyekuwa anajaribu kupinga kuna watu ambao walifungwa jela. Sasa mimi siwaambii Serikali mkawafunge wanaopinga mradi huu lakini niwaambieni wapuuzeni chapeni kazi tunahitaji Mradi wa Rufiji hydropower kwa ajili ya manufaa ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kushukuru kwa kupata fursa hii ya kuchangia na kushauri machache kwenye Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Kwanza nipende kumshukuru na kumpongeza kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro kwa ushirikiano ambao anaendelea kutupa sisi wananchi wa Kasulu, hususani Kasulu vijijini baada ya mvurugano mkubwa na TFS. Busara za Mheshimiwa Waziri zimetusaidia sana, tunamshukuru sana, sana, asiyeshukuru ni kafiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu miaka mitatu iliyopita kama sikosei miwili, kulitokea mlipuko huu wa ugonjwa wa corona yaani Covid 19. Ugonjwa ambao umefunga dunia kabisa na uliathiri sana, sana, mwenendo wa utalii duniani hata kwetu sekta ya utalii ilisinyaa sana. Sasa wakati huu ambapo tunajifunza kuishi na ugonjwa huu, nipende kwa dhati kabisa kumpongeza Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa juhudi na hatua anazochukuwa kuhakikisha kwamba anafungua Taifa letu ili kuhakikisha kwamba Taifa letu wageni wanakuwa na confidence ya kuja hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu tunajua sekta ya utalii key players ni foreigner hao ndio wakubwa. Sasa kama hawana confidence na nchi yetu, sasa kama hana confidence na njia ambazo tunazitumia kuhakikisha kwamba tunafungua nchi yetu au kufanya nchi kuwa salama, hapa utalii wetu utaendelea kusinyaa, ni lazima tukubali. Dunia imekubali kwamba namna ya kuweza kufungua dunia tena na shughuli mbalimbali za utalii ziendele ni namna ya kuwapatia watu chanjo, watu wapate chanjo ili wawe na confidence ya kusafiri kwenda sehemu mbalimbali, mtalii ajija hapa akipokelewa na mtu ambaye amepewa chanjo, naamini atakuwa na confidence kubwa zaidi kuliko kupokelewa na mtu ambaye hajapewa chanjo. Sasa katika hili kule mtaani tunasema, mama anaupiga mwingi sana katika upande huu wa kushughulikia suala la Covid-19.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina machache ya kumshauri Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro hasa kwenye utalii wa uwindaji. Kule kwangu Kasulu tuna kitalu cha uwindaji, sasa wakati wa Covid 19, utalii wa uwindaji umesinyaa sana, lakini wako wawekezaji wachache pamoja na kwamba utalii wa uwindaji ulisinyaa lakini wameendelea kuwa na sisi, vitalu vingi viko wazi kwa sababu ya Covid-19, lakini wako wachache ambao waliendelea kuwa na sisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande huu, ningependa kushauri yafuatayo ili kuhakikisha kwamba utalii wa uwindaji unaendelea kuwa na nguvu na unaendelea kutuletea mchango kwenye sekta ya utalii. Moja, ningependa tuwatie moyo wale ambao wamesimama na sisi wakati wa Covid 19. Kwa sababu ni ukweli usiopingika wengi wao wametengeneza hasara, wamelipa kodi, wamelipa kila kitu lakini watalii hawakuwa wengi kama ambavyo walivyotegemea, sasa lazima tuwape moja tuwatie joto.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ningependa kwenye mnada unaokuja hawa watu tuwape holiday wasishiriki mnada, waendelee kuwa na maeneo yale yale ambayo wamekuwa nayo, ili kuhakikisha kwamba wanaweza kurudisha zile gharama ambazo wameingia hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa sana kwa wakati huu ambapo tunapambana na ugonjwa hili, tujitahidi sana kuwaruhusu watu walipe kwa instalment. Kama mtu umemwambia kitalu unachomuuzia ni dola 80,000, basi ufanye alipe kwa instalment ili kwamba aweze kupata nafasi pamoja na mazingira magumu ya kiuchumi ya kuweza kulipia Serikali ipate mapato.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kengele imeshagonga.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba dakika moja tu, lipo la msingi.

NAIBU SPIKA: Kila mtu akiomba moja sitaweza, sekunde 30.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, moja muda wa watu wa kufanya mnada urefushwe. Haya mambo ya kumpa mtu mwaka mmoja halafu utegemee aendeleze kitalu kwa kuendelea kufanya uwekezaji haiwezekani, lazima tuongeze muda wa kufanya mnada. Ukimpa mtu umpe miaka mitano, miaka angalau kumi aweze kufanya uwekezaji, aendeleze kitalu vizuri. Kwa kufanya hivyo..

NAIBU SPIKA: Muda wako sasa umekwisha.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii ya kuchangia bajeti kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanza kabisa kwa uzito wake, nipende kuchukua fursa hii, Mwenyekiti jana Mkoani Mwanza kulitokea tukio zuri la kihistoria na la kuenziwa. Mheshimiwa Rais wetu mpendwa alipata muda wa kukaa na vijana wa nchi hii kutoka maeneo mbalimbali Mkoani Mwanza, akaongea nao kwa kirefu sana, lakini alitumia muda wake mwingi kuwaeleza imani kubwa aliyonayo kwa vijana wa nchi hii, lakini fursa ambazo zipo Serikalini, akatutia moyo vijana wa nchi hii lakini akatuhakikishia ulinzi katika harakati zetu zautafuta maisha na kujenga nchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kadi nyekundu ilitoka jana pale pale kwa watu ambao walionekana kwamba wanabeza juhudi za vijana za utafutaji. Sasa kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais lakini nashawishika kuwaomba vijana wenzangu Tanzania kote, kwamba ni wakati muafaka sasa kama ambavyo tulikuwa tunafanya kuhakikisha kwamba tunamlinda Mheshimiwa Rais wetu na kumtetea katika maeneo yote. Kwenye mitandao, kwenye matukio mbalimbali, tuhakikishe kwamba tunamlinda na kumtetea Rais wetu kwa kuwa anayo maono makubwa sana kuhusu vijana wa nchi hii.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa

MWENYEKITI: Taarifa.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe Mheshimiwa taarifa sio ombi ni amri kwa vijana. (Makofi)

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa naipokea. Vile vile nipende kumshukuru sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan wiki iliyopita nilipata taarifa kwamba ametupatia Jimbo la Kasulu Vijijini shilingi Milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa barabara za vijijini. Fedha ambazo nimeshajadiliana na meneja wangu wa TARURA kwamba tutachonga barabara ya kutoka Kata ya Kigembe kwenda mpaka Kata ya Rungwe mpya kwenda kufungua maana yake Tarafa ya Buyonga na Tarafa ya Heruchini. Kwa kweli tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hili ninamshukuru sana pia kwa shilingi milioni 600 za Ujenzi wa shule ya sekondari ambazo anatupatia Kasulu Vijijini fedha ambazo tumekubaliana tunakwenda kujenga kwenye Kata ya Karela, kata ambayo ina shule tatu za msingi sasa tunataka kuwapa shule ya sekondari ambayo ni zawadi kutoka kwa Mama Samia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nipende kumpongeza sana Mheshimiwa Mwigulu na timu yake kwa kazi kubwa ambayo wameifanya ya kuandaa bajeti. Ni bajeti ambayo imeonesha vyanzo mbadala vya mapato ukiachilia mbali ambavyo tumekuwa tukiendelea kubana walipa kodi kwa maana ya watumishi na wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumshauri au kumwongezea yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la watengenezaji wa matrela ya malori haya, mwanzo au miaka ya nyuma kidogo tulikuwa na watengenezaji zaidi ya 10 nchi hii, lakini leo hii wamepungua wamebaki watatu, kama sikosei tunao Super doll, AM sijui na mwingine yupi, lakini ziko kama tatu. Kwa nini wanapungua na hawa wanaweza wakafunga viwanda vyao ni kwa sababu zipo nchi ambazo watu wanaenda kununua huko matrela na kwa nini wanaenda huko?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanakwenda huko kwa sababu manufactures wa huko wa China nadhani kama kama sijakosea na Uturuki, wanapewa export levy na nchi zao asilimia 20 ya FOB. Sasa wanakuwa na uwezo wa kuuza matrela kwa bei ndogo sana, sasa mtu akinunua kule akija kwa bei ndogo, akija hapa Tanzania analipa import duty yaani asilimia 10. Sasa ukiangalia mtu akinunua gari za kutembelea IST kwa mfano, akija hapa Tanzania analipa import duty nadhani asilimia 20 sijui 25. Wakati huyo mtu hana mpinzani, hakuna mtu ambaye anatengeneza magari hapa Tanzania kwa maana IST na gari nyingine, lakini matrela haya ambayo wapo watengenezaji wa Tanzania wapo hapa Tanzania, unashangaa wanatozwa kidogo na hatimaye viwanda vyetu vinaendelea kupata wakati mgumu kwa sababu ushindani wa bei unakuwa ni mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba, hapa kuna chanzo kingine cha fedha moja tuongeze import duty kwenye matrela haya iende kuwa sawasawa na gari zingine tu za kawaida za kutembelea angalau asilimia 20. Hii italinda viwanda vyetu na hawa watengenezaji wa ndani na lazima wataongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio ya kwetu tu yapo mengine mengi matrela ambayo yanapita hapa kwetu kwenda kwenye land locked countries na wenyewe wanalipa asilimia 10 hapo import duty. Kwa hiyo tunayo nafasi ya kungeza fedha, tunayo nafasi ya kulinda viwanda vyetu, tunayo nafasi ya kufanya jambo hili ili kuongeza fedha katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo mwanya mwingine nataka nimshauri Mheshimiwa Mwigulu na timu yake, Kasulu sisi tunao walipa kodi wachache kwa maana ya watumishi ni wachache lakini na wafanyabiashara ni wachache. Hata hivyo, ipo fursa, tulianzisha miaka mitano iliyopita. Sisi kule kwetu baada ya Tanzania kuingia kwenye uchumi wa kati, Watanzania wa Kasulu wale wananchi wa Kasulu hawaendi tena kufanya kazi za mashambani, wanaofanya kazi za vibarua vya mashambani idadi yao imepungua. Sasa pale mara nyingi wanatumia watu kutoka nchi ya jirani ya Burundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu hakuna utaratibu ambao ni rafiki wale watu wanaotoka Burundi wanakuja na ni maarufu wako Kasulu. Ukitafuta data kutoka kwa watu wa Immigration Kasulu watakwambia. Yako maelfu ya watu wanatoka Burundi kuja kufanya kazi za mashambani. Sisi baada ya kuingia uchumi wa kati, lakini pia shule za kata zikajengwa, watu wa Kasulu awanaenda kusoma shule na wakimaliza shule wanaajiriwa, wengine wanajiajiri, wengine wanaenda mikoani kutafuta Maisha. Kwa hiyo ule utaratibu wa watu wa Kasulu kwenda kufanya kazi ya vibarua mashambani umepungua. Kwa hiyo manpower ambayo tunaitegemea sasa hivi ni nchi ya jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulianzisha utaratibu, ilikuwa miaka mitatu iliyopita, tukamshauri Waziri wa Mambo ya Ndani tuanzishe kituo kinachoitwa season immigrant pass ambayo akija hapa mtu wa Burundi ataweza kulipia Sh.30,000, aliyemleta atalipa Sh.60,000. Hawa watu ni wengi kuliko wafanyabiashara na watumishi wa Kasulu, hapa kuna fedha nyingi kuliko kodi ambayo tunaikusanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana sana Serikali ilitazame hili kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani. Mchakato ulishaanza nadhani Mheshimiwa Kangi Lugora aliusaini wakati ule, naomba tuuendeleze, kuna fedha nyingi sana hapa kuliko ambazo wanawabana wafanyabiashara. Juzi nimesikia, mpaka wafanyabiashara wamegoma kwa sababu wanakamuliwa Kasulu pale mpaka inakuwa ni too much, wamegoma. Akaenda Kamishna wa TRA kurekebisha mambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme, hapa kuna chanzo kingine cha fedha, nyingi sana mamilioni ya shilingi kutoka Wilaya ya Kasulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikumbushe jambo moja tu iko miradi inaendelea kwetu Mradi wa Barabara kutoka Buhigwe-Kasulu, Kasulu kwenda mpaka Nyakanazi. Ule mradi speed yake tunashukuru ipo vizuri, lakini iko miradi ya bonus ambayo tuliambiwa inakuja na hiyo barabara. Kwangu pale tuliahidiwa kujenga hospitali lakini na gari la wagonjwa ambayo ni zaidi ya bilioni mbili na milioni 400.

Ukienda Buhigwe, ukienda Kasulu Mjini wana ya kwao, ukienda Kakonko kwa ndugu yangu Mheshimiwa Kamamba yapo, ukienda Kibondo kwa dada yangu yapo, tunataka hii miradi sasa ianze kuletewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iletwe hela kwa sababu tuliambiwa kwamba utekelezaji wa ujenzi wa barabara utaendana na miradi hii ni mabilioni ya shilingi ambayo kama fedha zikitolewa kwa wakati Mkoa wetu wa Kigoma unakwenda kunufaika sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono bajeti, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii awali ya yote naunga mkono hoja zote mbili na ni Mjumbe wa Kamati ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nichukue fursa hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais kwenye ziara zake hizo za Ufaransa na Ubelgiji tumeona anasaini mkataba, wa mabilioni ya shilingi ambayo tunaamini yatakuja kwenye Taifa letu na hatimaye itakuwa ni hatua muhimu sana kuwasaidia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaongelea maeneo mawili kwenye taarifa yetu eneo la kwanza ni kwenye kiwanda cha viuatilifu kile ambacho kipo kwenye Mkoa wa Pwani. Naanzia hapo kwa sababu ni kiwanda mahususi ambacho kilianzishwa kwa ajili ya kutokomeza malaria na kwa miaka kumi, ukianzia mwaka, 2010 mpaka mwaka, 2020 tumepoteza watanzania zaidi ya 70,000 kwa sababu ya ugonjwa wa malaria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya ni Majimbo kadhaa ya uchaguzi tumeyapoteza. Mwaka 2015 NDC Shirika letu lilichukua mkopo ambao ni takribani shilingi bilioni 50 kutoka Hazina kwa ajili ya kuanzisha ujenzi wa kiwanda hiki. Kiwanda ambacho kilijengwa na kukamilika mwaka 2017 kiwanda walisaini mkataba na Wizara ya Afya kwa maana ya kwamba Serikali, kupitia halmashauri itakuwa inanunua viuatilifu hivi na kwenda kupulizia huko kwenye mazalia ya mbu ili kutokomeza mbu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikueleze ule mkataba haujatekelezwa, kiwanda hakiuzi viuatilifu, ni kama kimetelekezwa, tunajiuliza kuna hujuma au kuna nini katika hili? Over 50 billion! Serikali inatumia mabilioni ya shilingi kila mwaka kwa ajili ya kupambana na malaria. Kwa nini tusiende kununua viuatilifu hivi tukapuliza hatimaye tuondokane na tatizo la malaria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jamaica wameondokana na malaria kwa sababu ya kutumia teknolojia hii ambayo walitupa nasi, tulinunua kwao. Kiwanda kile hakina faida hiyo tu kwa maana ya kwamba ni viuatilifu vya kupambana na malaria. Kamati tumetembelea pale walituambia kwamba kiwanda kile kina uwezo wa kutengeneza viuadudu (pesticides). (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu inatumia mabilioni ya shilingi kila mwaka kwa ajili ya kununua viuadudu kwenye masuala mbalimbali, nchi hii inatumia bilioni 57 kila mwaka kununua viuadudu kwa ajili ya zao la pamba, inatumia bilioni 50 kwa ajili ya kununua viuatilifu kwa ajili ya zao la tumbaku na inatumia karibu bilioni 100 kila mwaka kwa ajili ya kununua viua wadudu kwa ajili ya zao la korosho. Ni mabilioni haya ambayo kila mwaka tunayapeleka nje ya nchi wakati tuna kiwanda na teknolojia hapa, kama tukikipa uwezo, tukawekeza pale, Serikali isikitelekeze, tunaweza tukaokoa mabilioni ya shilingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nigusie kidogo kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Kwanza Mheshimiwa Naibu Spika hongera sana kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii tunajua wanafanya biashara, lakini wanaenda kuwekeza zaidi kwenye real estate mabilioni ya shilingi wanapeleka yote kwenye real estate, wanajenga majengo hata majengo yenyewe hawayamalizi, wanaenda kujenga majengo porini kama lile la Dege Beach kule Kigamboni ambayo return yake hakuna, wameshindwa na ku-prove failure kwenye real estate. Hela za Watanzania zimewekwa kule, zimefia kule. Sasa sijui ni woga, wakitoka hapo wanaenda kwenye mambo ya investment kwenye mambo ya bonds hapo wanashindana na Wabunge na Watanzania wengine kwenda kununua bonds! Hawa wanapaswa wawaze vitu vikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, real estate ina players wengi, TBA wapo humo ndani, National Housing wapo humo ndani na akina Musukuma wapo humo ndani, akina Kishimba wapo humo ndani na wawekezaji wengine wengi, waachane na real estate, waende kuwekeza kwenye vitu ambavyo vina faida kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalo tatizo la mbolea hapa Tanzania kila mwaka, NSSF wakiamua kumaliza tatizo hili wanaweza, watujengee kiwanda kikubwa cha mbolea hapa ambacho kinamaliza shida ya mbolea Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo shida ya sukari, tunazo shida kwenye mambo mbalimbali, kwa hiyo nadhani mashirika haya…

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa. Mheshimiwa Musukuma.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ninapenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba hata hizo real estate zinazowekezwa na Taasisi za Serikali zinakuwa nje ya soko kwamba tunayo maeneo ndani ya mji ambayo wanaweza wakajenga na kupata wapangaji, wanazitoa wanaenda kuzi-dump ili wapige deal halafu na nyumba hazipati wateja. (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Vuma taarifa hiyo.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea, naamua kukubali kwa sababu ni Mheshimiwa Musukuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme, hawa watu wajielekeze kwenye vitu, leo hii Mama amewapa hela nyingi sana, juzi tu hapa, walikuwa na madeni Serikalini, kawapa over two trillion siyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, wanatakiwa waende kumsaidia kutengeleza ajira, waende kwenye investment, business model ambayo inatengeneza ajira mbalimbali kwa Watanzania, haya mashirika yanayo nafasi ya kutusaidia, kumsaidia Mama kutengeneza ajira kwa Watanzania. Kwa hiyo waachane na vitu vidogo vidogo hivi ambayo hata vyenyewe vimewashinda, waende kuwekeza kwenye mambo makubwa ambayo yataleta faida ya kiuchumi pia na kuongeza ajira kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono tena hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii nami niweze kuchangia kuhusu taarifa za Kamati ambazo ziko mbele yetu. Awali ya yote napenda kuishukuru Serikali kupitia Waziri wa Fedha pamoja na Waziri wa Kilimo. Kama taarifa yetu ya PIC ilivyojieleza, tulipata nafasi ya kuwaita kwa ajili ya kufuatilia maazimio ambayo tuliyaweka hapa ya Serikali kulipa deni kwenye Sekta Ndogo ya Bodi ya Pamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, waliweka wazi kwamba wanakamilisha uhakiki na wakasema mpaka kufikia mwezi wa tatu uhakiki utakuwa umekamilika na wataingiza kwenye mwaka wa bajeti unaokuja kwa ajili ya kulipa. Nawapongeza, lakini niseme tu Serikali ijipange ihakikishe kweli kwenye bajeti ijayo inaingiza deni hili la sekta ndogo ya pamba. Kwa nini? Kwa sababu sekta ndogo ya pamba imedorora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu ilipotokea ile patashika ya mwaka 2019, baada ya Soko la Pamba Duniani kucheza, na hatimaye watu wakaingiza mitaji yao kwa promise ya Serikali kwamba itaweza kutoa ruzuku, ukweli ni kwamba Serikali iliposhindwa kutoa ruzuku upatikanaji wa pembejeo umekuwa ni shida. Kwa sababu kuna deni la zaidi ya Shilingi bilioni 80 la pembejeo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata wanunuzi wenyewe wamesinyaa kuendelea na shughuli hiyo, kwa sababu yako madeni makubwa ambayo ni zaidi ya Shilingi bilioni 100 Serikali inapaswa kulipa ili kuhakikisha kwamba sekta ndogo ya pamba inaendelea kustawi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye taasisi yetu, Shirika la TANAPA. Jambo la kwanza, Hifadhi ya TANAPA labda kwa uelewa tu, awali ilikuwa na hifadhi 16 ambazo zina kilomita za mraba zaidi ya 57,000. Zikaongezeka mwaka 2019 kama sikosei, zikaongezeka hifadhi sita ambazo zina kilomita za mraba 47,000. Ikafanya jumla ya hifadhi zote zikawa 22 ambazo zina kilomita za mraba zaidi ya 100,004.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni ongezeko zaidi ya asilimia 45. Cha kushangaza sasa, badala ya Serikali kuwa inaongeza fedha za maendeleo na matumizi ya kawaida, imekuwa inazipunguza kila mwaka. Cha ajabu hicho! Ukiangalia kwa mfano, kuanzia mwaka 2019 zilipoongezeka hifadhi sita mwaka 2019 Serikali ilitenga shilingi bilioni 70 kwa ajili ya matumizi ya maendeleo kwenye Shirika la TANAPA. Mwaka uliofuata wakapunguza shilingi milioni 500, yaani ikawa ni shilingi bilioni 69.5. Mwaka uliofuata wakapunguza zaidi wakatenga shilingi 64,500,000,000/=. Mwaka huu tulionao wamepunguza zaidi, wametenga shilingi bilioni 60.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa unafikiria, ni kitu gani hiki? Yaani umeongeza ukubwa wa kazi kwa TANAPA kutoka hifadhi 16 mpaka 22 ongezeko la zaidi ya asilimia 45, badala uwaongezee fedha, wewe unapunguza. Mimi sijui tunafanya kitu kitu hapa! Ni kituko ambacho hakivumiliki. Wamekuja kwenye Kamati wanalialia pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima Serikali ichukue hatua. TANAPA tuna kila sababu ya kuiongezea fedha. Kwanza, ni taasisi za kimkakati. Hawa wanasimamia zaidi ya asilimia 11 ya eneo la nchi yetu. Bwawa la Mwalimu Nyerere liko chini yao pia. Kuna Askari zaidi ya 120 ambao wanalinda pale Bwawa la Mwalimu Nyerere. Wanaimarisha ulinzi na usalama. Hawa hawana nyumba za kulala, hawana usafiri wa uhakika. Bwawa ambalo lina matrilioni ya Shilingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama haitoshi, TANAPA tunajua imeajiri Watanzania wengi sana; tunajua TANAPA ni chanzo cha mapato kwa Serikali; tunajua TANAPA kupitia hifadhi zake na shughuli zake ni chanzo kikubwa cha fedha za kigeni; pia TANAPA inalinda urithi wetu na utambulisho wetu kupitia mbuga zetu mbalimbali na vivutio vya kiutalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kwamba tuna kila sababu ya kuongezea fedha shirika hili. Kama tunaihitaji TANAPA kwa maana ya hifadhi zake ziendelee kuwepo, urithi wetu uendelee kuwepo, utambulisjho wetu uendelee kuwepo, tuendelee kupata mapato, ajira za Tanzania, tuendelee kusimamia kikamilifu hii asilimia 11 ya nchi yetu, lazima tuwaongezee fedha TANAPA ili waendelee kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TANAPA mahitaji yao; tuliwahoji siku ile walivyokuja kwenye Kamati. Wao wanaomba fedha za maendeleo shilingi bilioni 120 kwa ajili ya vifaa vya maendeleo. Wanaamini wakipata fedha hizi watafanya miradi mikubwa ambayo itaboresha sana mazingira ya hifadhini na hatimaye kuongeza watalii kwa kiasi kikubwa sana. Hata hivyo, wanahitaji zaidi ya shilingi bilioni 220 kwa sababu tumewaongezea eneo la kufanya kazi zaidi ya asilimia 45. Wanahitaji shilingi bilioni 222 kwa ajili ya matumizi ya kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashindwa kuelewa, yaani Serikali kupitia Mheshimiwa Rais, amefanya kazi nzuri sana ya ku-promote utalii wa nchi hii kupitia Royal Tour na watalii wameongezeka kweli kweli, wanatiririka kweli kweli! Tume- overcome hata ile challenge ya Covid, imeisha na watalii wanazidi kuja kutokana na initiative ambayo Mheshimiwa Rais ameifanya kupitia Royal Tour. Sasa Watendaji wa Serikali wanashindwa vipi kuhakikisha kwamba wanaweka mazingira mazuri ili hao watalii wakija wakutane na mazingira ya kisasa zaidi ambayo ni rafiki, wazidi kuja Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Wabunge wote, naomba sana tuweze kuungana kuibana Serikali kwa kuishauri iongeze fedha kwa ajili ya TANAPA ili TANAPA wawe na uwezo wa kusimamia na kuendesha hifadhi zake vizuri kwa ajili ya maslahi mapana ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwashukuru sana TANROADS kwa kazi nzuri sana ambayo wanayoifanya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri, muda wako umekwisha.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kunipa uhai mpaka kufika leo. Pia napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuwafanyia Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwenye Sekta ya Afya, sisi Kasulu tumeendelea kulamba asali kama alivyosema Mzee Makamba juzi. Tumepokea chini ya Mheshimiwa Rais Samia zaidi ya Shilingi bilioni 3.1 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kasulu DC. Pia tumepokea Shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya Kitanga, tumepokea Shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuboresha Kituo cha Afya cha Kurugongo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumepata pia Shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba ambazo ziko MSD. Hapo nataka nigusie kidogo; Mheshimiwa Ummy yuko hapa; kwanza napongeza maamuzi ya Mheshimiwa Rais kufanya overhaul kwenye MSD na kupata Mkurugenzi mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mkurugenzi mpya na ninaamini kwamba ataenda kufanya marekebisho pale ambapo kulikuwa na changamoto ili kuhakikisha kwamba vifaatiba hivi na dawa vinafika kwa wakati. Nimtie moyo tu kwamba yeye sasa hivi ndio Mkurugenzi wa MSD, kwa hiyo, asiogopeogope. Pale ambapo kuna changamoto ambazo zinatakiwa kufanyiwa mabadiliko kisheria, amwambie Waziri atuletee sisi hapa ndio Wabunge tunaotunga sheria, turekebishe kuhakikisha kwamba hatuna changamoto za kisheria ambazo tunaweza kuzipitia.

Mheshimiwa Spika, Kasulu vijijini tunayo changamoto ya watumishi. Mheshimiwa Waziri sisi tuna watumishi 192 peke yake. Tunazo Zahanati 32 Vituo vya Afya sita na Hospitali ya Wilaya moja, lakini wote hao wanahudumiwa na watumishi 192, ambayo ni sawasawa na asilimia 22 tu ya mahitaji yote. Chonde chonde, naomba sana Kasulu Vijijini katika jambo hili tupewe jicho la kipekee sana, kwa sababu watumishi wanafanya kazi sana, wanachoka. Tuna sekta kama upande wa mionzi, tuna mtumishi mmoja tu ambaye anahudumia halmashauri nzima. Kwa hiyo, naomba sana jambo hilo litazamwe.

Mheshimiwa Spika, suala la wizi wa dawa, kwanza linafanya bima yetu ya afya kubeba mzigo mkubwa sana, kulipa dawa ambazo watu hawajatumia. Pili, inachafua mno Serikali yetu. Majengo mazuri, lakini hayana dawa. Mwananchi haendi pale kwa ajili ya kutazama majengo, anaenda kwa ajili ya kutafuta huduma. Sasa nina ushauri kidogo, huwezi kuzuia wizi wa dawa kwa kufanya tu ziara za kushtukiza hospitali. Utafanya ngapi?

Mheshimiwa Spika, huwezi kuzuia wizi wa madawa kwa kusema kwamba ile sheria ambayo tuliipigia kelele kidogo kwamba maduka ya dawa yajengwe mbali na zahanati au na Kituo cha Afya, Hapana. Kwa sababu yakijengwa hapo hapo au mbali, wizi kama upo, upo tu. Hoja yangu ni kwamba, katika dunia ya leo ambayo teknolojia imekuwa kubwa sana, Mheshimiwa Waziri unayo fursa ya kuja hapa kutuomba hela tukupe fedha za kutosha uweke mifumo thabiti ya IT ili kuweza kuondoa wizi wa dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda huko kwa wenzetu, suala la wizi wa dawa limeshaondoka, siyo kwa sababu ya vitisho wala kauli mbalimbali, Hapana. Ni kwa sababu wameweka njia ambazo ni za kisasa za mifumo ya kiteknolojia kwa ajili ya kulinda dawa. Wewe Mheshimiwa Waziri kipindi ukiwa ofisi kwako huwezi kujua kuwa Kasulu Vijijini kuna kiasi dawa kiasi gani? Siyo mpaka upige simu, uki-click tu unaona track. Njoo uombe hela hapa Bungeni, tukupitishie uende ukafanye. Najua ni investment kubwa, lakini ukafanye kwa ajili ya maslahi mapana ya Watanzania, otherwise naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia leo kwenye Bunge lako Tukufu. Nikushukuru pia wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais na wasaidizi wake, kwa maana ya Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kuhakikisha kwamba Wilaya ya Kasulu au Mkoa wa Kigoma kwa ujumla tunapata kiwanda cha kuzalisha sukari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hapa kwa sababu kwa miaka mingi iliyopita Wabunge wa Mkoa wa Kigoma tume-push agenda hii humu humu Bungeni na hatimaye Serikali iliweza kuweka mazingira mazuri na hatimaye mwekezaji wa Mufindi Papers au Kasulu Sugar ameanza shughuli zake pale, wamepanda miwa na ujenzi wa kiwanda unaendelea. Tunaamini muda siyo mrefu Wilaya ya Kasulu kutakuwa na kiwanda kikubwa sana cha sukari katika Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapo hapo nimpongeze Mheshimiwa DC na Mkurugenzi kwa kazi nzuri waliyofanya kuhakikisha kwamba wana-manage changamoto ndogo ndogo ambazo zilikuwa pale kwenye vijiji husika, hasa wakati wa kupata ardhi na mambo mengine, na kuhakikisha kwamba muwekezaji anaendelea na shughuli zake vizuri.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, nimeona kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri, anasema Benki ya Kilimo imetoa bilioni 47 kwenye mwaka wa fedha uliopita kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya kuchakata mazao na kuongeza thamani ya mazao.

Mheshimiwa Spika, Benki ya Kilimo inafanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha kwamba inawezesha viwanda kwa kuchakata mazao mbalimbali kwenye kilimo na uvuvi. Sasa tumeona kuna initiative nyingi sana za Serikali kwenye kilimo na sehemu zingine, lakini bila kuwa na viwanda ambavyo vinachakata mazao hayo ni ukweli usiopingika kwamba kilimo chetu hakiwezi kuwa na tija na mkulima hatuwezi kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kamati yetu ya PIC ilipendekeza kwenye taarifa yake ya mwaka uliopita kwamba Serikali iiongezee mtaji Benki ya Kilimo, bilioni 100. Ni vizuri, tunataka kujua kama Bunge au wananchi Serikali imefikia wapi katika kutekeleza jambo hilo? Kwa sababu kwa kufanya hivyo tunaamini watu wengi watakopeshwa. Hata wa Mkoa wa Kigoma tumepata fursa ya kupewa, kuna mwekezaji amepewa mkopo tunajenga Kiwanda cha Kukamua Mawese Mkoa wa Kigoma, tulikuwa hatuna.

Mheshimiwa Spika, Dodoma hapa wamejenga Kiwanda cha Kukamua Mchuzi wa Zabibu. Kwa hiyo lazima tuimarishe, lazima Serikali iwape fedha ya kutosha Benki ya Kilimo ili iweze kuhakikisha inawezesha ujenzi wa viwanda kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, na mimi nitagusa suala hili la cement kidogo. Kwa nini nagusa; naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize kwa makini sana. Cement kwa Dar es Salaam inauzwa mfuko mmoja shilingi 14,000. Cement Kigoma au Kasulu Vijijini mfuko mmoja unauzwa shilingi 28,000, yaani ni mara mbili ya Dar es Salaam. Sasa tumepiga makelele sana kwa maana ya kuishauri Serikali kuendelea kuongeza production, yaani uzalishaji na Serikali imechukua hatua ya kushawishi wawekezaji nje ya nchi na ndani ya nchi ili wawekeze kwenye viwanda vya cement ili cement na kule Mbeya, kule Kigoma iweze kushuka iwe kama Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, sasa amepatikana muwekezaji kwenye kiwanda ambacho kinasuasua anataka kuleta over one trillion halafu inakuja movement ya kupinga jambo lile kwa sababu kuna technicalities eti hazikufuatwa. Sasa nimefikiria unakumbuka hata wakati tunaanza ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere walikuja watu hapa wakasema tumekiuka Sheria za Mazingira. Wakati tunaanza ujenzi wa SGR walikuja watu wakasema mnakiuka moja, mbili, tatu. Nataka niseme nampongeza Mheshimiwa Waziri na FCC kwa maamuzi ya kijasiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi hii tumekwamakwama kwa sababu ya kukosa maamuzi wakati mwingine. Vitu vidogo vidogo unakuta vinamzungusha mwekezaji mpaka anaamua kurudi kwao, hatuwezi kwenda namna hiyo, no thank you. You can not reject wawekezaji wa over one trillion eti kwa sababu kuna technicalities za mwanzo hazijafuatwa. Nilidhani wakati tunachangia hapa, tulipaswa tumpongeze kwanza Waziri, halafu tutoe ushauri wa namna ya Kwenda, tuwe supportive sio ku- discourage, eti unakataa one trillion unaijua wewe vizuri, unaijua one trillion vizuri wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hela ni ngumu jamani, hatukubaliani. Lazima huyu mwekezaji atiwe moyo, lazima huyu mwekezaji apewe nguvu, apewe mwongozo wa kutosha kwa maslahi ya Watanzania, hasa wa Kasulu Vijijini ambao wananunua cement kwa shilingi 28,000 wakati Dar es Salaam wananunua kwa shilingi 14,000 we cannot accept this.

Mheshimiwa Spika, hongera Mheshimiwa Waziri anafanya kazi vizuri, lakini sasa ukiangalia hofu ya watu, nilijaribu kuongea na watu hasa wa Mkoa wa Tanga ambako ndio kuna kiwanda chenyewe. Hofu yao kubwa wanasema kwamba huyu akinunua hiki kiwanda kinaenda kufa na walitoa mfano wa baadhi ya viwanda ambavyo vimeshakufa. Wakasema viko viwanda kadha wa kadha ambavyo vimekufa pale.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kujua, FCC kwenye mashauri yao wana ruling za aina tatu. Moja kumpa mtu yaani anunue au a-merge katika jambo hili. Jambo la pili, unampa bila masharti, unampa tu bwana tumekubali, hakuna masharti yoyote, nunua. Jambo la tatu, unampa na masharti, masharti haya ndio ambayo yanaweza kusaidia kumlazimisha ili production ya eneo lile iendelee na kiwanda kisifungwe au kumkatalia. Sasa naamini Waziri atakapokuja hapa atakuja kuwaambia vizuri, huyu mtu anakubaliwa kwa misingi gani, anapewa bila masharti au anapewa mashati. Ningeshauri apewe kwa masharti kwa maana ya kwamba tuwe na uhakika kwamba tukimpa kiwanda kile haendi kukifunga, anaenda kukiendeleza, hivyo, ajira zinaendelea kuwepo na cement ya kutosha inakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara muhimu, Wizara ambayo imebeba maisha ya watanzania walio wengi. Awali ya yote nipongeze Serikali Kupitia Mheshimiwa Rais, kwa kuendelea kuongeza bajeti ya Wizara ya Kilimo. Ni wazi kwamba kwa kufanya hivyo wanagusa watanzania walio wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaenda moja kwa moja kwenye mchango wangu. Jambo la kwanza; Jimbo la Kasulu Vijijini lina kata 21, kata 10 kati ya 21 wanalima pamba. Ukienda kwenye Kata ya Asante Nyerere, Kata ya Rungwe Mpya, Kigembe, Pwaga, Shunguliba, Nyamidaho, Kitagata, Kurugongo na Lusesa, kata kumi, kata zote hizi ni wakulima wa pamba.

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali tangu mwaka 2019 mpaka leo 2023 imeweka baridi kwenye sekta ndogo ya pamba. Baridi kivipi? Kuna madai ya key players kwa maana ya makampuni ya ununuzi wa pamba lakini na makampuni ambayo yana–supply pembejeo wanadai Serikali zaidi ya bilioni 102 kwa zaidi ya miaka minne sasa Serikali inadaiwa, imeshikilia pesa hiyo haijawalipa fedha zao. Kwa kufanya hivyo, kumefanya sekta ndogo ya pamba iweze kuathirika na kusinyaa. Wananchi kule ndio ambao wanateseka kwa sababu hawa ndio key players. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumefanya vikao mara kadhaa na hata hapa Bunge lako liliazimia kwamba Serikali inapaswa kulipa fedha hizo. Tunataka tujue wakati waziri akija hapa kwenye majumuisho atueleze ni lini Serikali italipa fedha hizi za key players hawa kwenye sekta ndogo ya pamba ili kuchangamsha sekta hiyo otherwise hatutakubaliana. Hilo ni jambo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nichangie kuhusu Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, Mheshimiwa Waziri, unisikilize kwa umakini, CPB ilikuwa ni taasisi ambayo inaenda kufa kabisa it was a loss-making company. Sasa hivi imeanza kutengeneza faida na inakwenda vizuri, lakini ziko taratibu ambazo bado zinaishika. Tumewasikiliza kwenye Kamati yetu ya PIC mara kadhaa. Hawa CPB wanafanya biashara kama wafanyabiashara wengine, wana–competitor wengi tu kwenye kuuza unga, kwenye kuuza sijui nini, kwenye kuuza mafuta, kwenye yote wanayoyafanya wana competitors wengi.

Mheshimiwa Spika, sasa kuna changomoto ya kwanza ni kuhusu mtaji. hawa watu kwa sababu wanafanya biashara na wanapata faida wala hawahitaji Serikali ichukue mtaji iwape ila iwawekee utaratibu mzuri wakitaka kukopa fedha.

Mheshimiwa Spika, CPB wakitaka kukopa fedha kwa ajili ya biashara wanatakiwa kwenda kuomba kibali. Yaani bodi ya CPB haina mamlaka wala nguvu ya kuweza kwenda kukopa, yaani kwenda kukopa benki mpaka waombe kibali kutoka Wizara ya Fedha, mchakato ambao huwa unakwenda mpaka miezi mitano au sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sasa wakati kuna competitor wengine wakitaka mtaji wao wanakwenda benki wanakopa wana-invest kwenye biashaara sisi taasisi yetu hii lazima kwanza tusubiri miezi sita. Yaani bodi ilishapanga kukopa, imepitisha inaenda kwanza Wizara ya Fedha, unasubiri sijui miezi mitano au sita ndipo majibu yaje wakope.

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuisaidia taasisi hii. Kama tutataka kumsaidia Mheshimiwa Waziri taratibu hizi zirekebishwe, hawa watu wawe na uwezo wa kwenda kukopa. Bodi ikshaidhinisha wawe na uwezo wa kukopa, wakikopa tutakuwa tunafungua minyororo ambayo tumewafunga na tutakuwa na spidi nzuri sana kwenye ku- compete na wengine ambao wako kwenye soko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa ubunifu wake wa wakugusa sasa wakulima wadogowadogo kupitia bajeti yake ya mwaka huu. Nimesoma kwenye ukurasa wa 138 wa bajeti yake; kwamba anakwenda kujenga miundombinu kweye kila halmashauri. Kila halmashauri itachimbiwa kisima kirefu, kwa kuanzia, kwa hiyo watachimba visima 184. Pia amesema atawawezesha wakulima, yaani kila kisima kimoja kitatumiwa na wakulima 150, kila mkulima atapewa eka mbili. Kwa hiyo zaidi ya ekari 69,000 zitaendelezwa, hii ni hatua kubwa sana. Hata wale ambao walikuwa wanalalamika kwamba BBT haijachukua vijana wao, sasa unakuja mradi ambao kila halmashauri, kwa kuanzia, ina uwezo wa kuwa na watu au wakulima 150 ambao watawekewa utaratibu mzuri na hatimaye waweze kujiajiri, huu ni mwanzo mzuri. Ninaamini kila mwaka utakuwa unazidi kuongeza fedha ili badala ya kuchukua wakulima 150 uende mpaka 500 na zaidi katika kila halmashauri ili kuhakikisha kwamba wakulima tunawasaidia; hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Benki ya Kilimo, Benki ya Kilimo tulishasema hapa pia, lilishaweka Azimio la Bunge; kwamba wapewe bilioni 100 ili kuwea ku-bust mtaji wao waweze kuwafikia watu wengi. Kila mtu anasema Benki ya Kilimo inafanya vizuri, wengine wanasema hatujakopeshwa; ni kwa sababu wanania ya kukopesha lakini mtaji ni mdogo.

Mheshimiwa Spika, mimi najifikiria, kwa nini Benki ya Kilimo, yaani iwe chini ya Wizara ya Fedha, why? Hili Serikali mkalifikirie vizuri. Yaani kwa nini isiwe Wizara ya Kilimo huko huko? Yaani Benki ya Kilimo iko Wizara ya Fedha, sidhani kama kuna ulazima sana Benki ya Kilimo iende kuripoti kwa Waziri wa kilimo.

Mheshimiwa Spika, hii inaweza kusaidia sana kuepusha baadhi ya delaying communication na maamuzi, wala hakuna shida yoyote. Tunashudia kuna baadhi ya Wizara hapa zinamiliki vyuo; kwa nini wasiseme kwamba chuo cha kilimo ki-repot kwenye Wizara ya Elimu? Mbona kina-report kwa Wizara ya Kimo wenyewe? Chuo cha Biashara kina- report kwenye viwanda na biashara; kwa nini kisi-report kwa Wizara ya Elimu? Kwa hiyo hii nayo inawezekana. Wizara ya Kilimo wapeni benki yao ili kupunguza hizo delaying za communication kati ya Wizara na Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia kidogo kwenye Wizara ya Maji.

Kwanza niseme tu Wizara hii imesheheni vichwa sana kuna brain kubwa sana kwenye Wizara ya Maji kuanzia kwa Mheshimiwa Waziri mwenyewe ndugu yangu Mheshimiwa Aweso, msikivu, mchapakazi ana brain ubunifu wa kutosha, usimamizi mzuri lakini Naibu Waziri wake Mheshimiwa Maryprisca, timu Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu wote wako sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye mchango. Jambo la kwanza nishukuru sana Serikali kupitia kwa Mheshimiwa Rais na Waziri na Wizara kwa ujumla kwa miradi mingi ambayo wameendelea kuniletea jimboni kwangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokea mradi kwenye Kata ya Rusesa kata ambayo ilikuwa na shida kubwa sana ya maji mradi ambao kwa ujumla wake zinahitajika milioni 984 lakini nimeishapokea milioni 566 kwa hiyo, bado wakiniongezea milioni 300 namalizia ujenzi wa tank kuweka na sora na pampu ili wananchi wa Kata ya Rusesa wapate maji ya kutosha

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nyamnyusi nimepata milioni 977, Kagera Nkanda bilioni 1.300, Mvugwe milioni 353, Chekenya milioni 817, Kaboranzuri milioni 962 hii siyo hatua ya kubeza nashukuru sana sana wananchi wa Kasulu wanashukuru sana sana hata leo asubuhi nimekutana na Mheshimiwa Profesa Ndalichako siyo mbaya kwa sababu ni Waziri mmemfunga mdogo hawezi kuzungumza lakini alikuwa anafurahi sana kwa sababu mradi wake mkubwa wa maji Kasulu Mjini umeanza kutekelezwa angekuwa na yeye anaweza kuzungumza angezungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo la kwanza nataka Waziri unisikilize vizuri sana, Kigoma tunahitaji Mradi wa Maji wa Ziwa Tanganyika yaani kama kuna kuna legacy broo utaiacha ukiwa kama waziri ni kuhakikisha kwamba tunapata Mradi wa Maji wa Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mradi unajua URUWASA unaendelea na uchambuzi wa awali na wanasema chanzo kitakuwa kwenye kitongoji cha Shakachakara kijiji cha Kabwera Kata ya Nsimbo halafu tenki kubwa litajengwa Heru Juu Kasulu hii ukijenga tenki pale kama jina lake linavyosema anavyosema Heru Juu maana yake ni sehemu ambayo ina muinuko mkubwa. Maji unaweza ukayatupa kwenda wilaya yeyote Kakonko, Kibondo, Kasulu yenyewe, Kigoma Vijijini, Uvinza kote itaenda mpaka Kaliua na Sikonge kote. Kwa hiyo, nakuomba brother, is a very very big project hata Katavi watapata mpaka Rukwa. Tunaomba sana utusaidie sana sana, kwa kuanzia angalau mwaka ujao wa bajeti tuone kuna usanifu unaanza please over please. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye Mfuko wa Maji wa Taifa. Kwanza hapa nimpongeze bila kumung’unya maneno CEO wa Mfuko wa Maji tena kwa bahati mbaya anakaimu sijajua nyiye mtajua mnavyofanya lakini tumewaita mara kadhaa kwenye kamati tukaangalia progress zao ni ukweli usiyopingika mfuko wa maji umepeleka fedha nyingi sana kwenye kila kona ya nchi hii na kama haitoshi miradi ile hasa ambayo ilikuwa ni kichefuchefu wewe unafahamu umekuwa Waziri. Mfuko wa maji umekusaidia kuikwamua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nisema la kupongezwa kubwa sana kwenye mfuko wa maji ni hili la ubunifu wao wa kukopeshwa mamlaka kubwa za maji zile ambazo zinajiendesha kwa faida. Aingii akilini eti Waziri uumize kichwa eti kutafuta hela ukawape DAWASA no thank you, DAWASA database yao ya walaji wa maji kubwa purchasing power watu wa Dar es Salaam ni kubwa iko wazi huwezi kuwapelekea hela za ruzuku wale. Wale wanajiendesha kwa faida kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanakopeshwa na mfuko wa maji zile hela ambazo mnazipeleka za ruzuku zile zipeleke Kasulu, zipeleke Kibondo, zipeleke Uvinza, zipeleke Kigoma Vijijini yes lakini haya ma–giants hawa wakopeshwe kwa sababu wanajiendesha kwa faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatutegemei kuona unawapelekea kama kwa ndugu yangu pale Mwanza na RUWASA inajiendesha kwa faida kubwa sana naamini wanaweza kukopeshwa na mfuko wa maji wakawa wanalipa. Kwa hiyo, nipongeze sana ubunifu huo lakini tuongezewe pesa sasa mfuko wa maji ili uendelee kukwamua miradi mingi ambayo haijakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wameguswa kuhusu DUWASA. DUWASA sisi tumewasimamia kama Kamati ya PIC. DUWASA tutawapiga tu madongo bure tunataka Wizara iwasaidie kuongeza miradi ili production ya maji iwe kubwa. Kwa sababu baada ya ile ongezeko la watu Serikali ilivyohamia Dodoma wanasema production yao nusu ya mahitaji ya Mji wa Dodoma sasa unawezaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo nadhani wanajitahidi angalau tunakuja hapa tumeoga, tunakuja tumefua suti zinakaa vizuri I am telling you. Lakini katika hali ya kawaida production fifty percent ya mahitaji. Mradi kama huu ambao nimekuona Mheshimiwa Aweso juzi unaenda kuzindua Nzuguni ya vile midogo midogo ya dharula ifanyike wakati tunasubiri mradi mkubwa wa maji kutoka wapi? Ziwa Victoria kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Aweso jitahidi sana kuhakikisha kwamba unawasaidia watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Aweso pale ninae Kaimu Manager wa RUWASA wa Wilaya ya Kasulu Kijana kama wewe, anachapa kazi vizuri japo ana gari bovu kweli kweli kuliko watumishi wa Serikali wote Wilaya ya Kasulu. Kijana anajitahidi sana kweli kweli lakini bado anakaimu, nimekwambia mara mbili mara tatu moja ya jambo la kufanya watu wafanye kazi kwa ufanisi mkubwa ni kuwapa haki yao wanayostahili, yule kijana anatusaidia sana, sana Kasulu sana sana Kasulu hebu mpeni haki yake anatusaidia sana Kasulu, Madiwani wanampenda, Mbunge nampenda, Watumishi wanampenda anasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii miradi ameisimamia kwa nguvu kubwa ni mbunifu anashirikisha sasa anakaimu leo mwaka wa pili hata yenyewe ile sheria ya kukaimu si miezi sita peke yake Mheshimiwa Aweso.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia kwenye Bajeti hii ya Fedha. Awali ya yote nikupongeze Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu na Naibu Waziri lakini pia na Kamishna wa Kodi, Ndugu yangu Kidata kwa sababu ya kazi kubwa ambayo mnafanya katika Taifa hili ya kukusanya kodi. Kimsingi iko wazi kwamba ni ngumu sana mkusanya kodi kuwa popular kwa hiyo, wakati mwingine mkipigwa mawe mvumilie tu, Taifa linajua kazi kubwa ambayo mnaifanya na tunatambua kwamba mmebebeshwa mzigo mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nipende kuanza na suala la microfinance; suala la microfinance huko kwa wananchi ni tatizo kubwa sana. Nakumbuka kama miaka miwili iliyopita ilikuja sheria hapa tutarekebisha sheria ili kupunguza angalau makali, kuanzia kwenye riba ambayo microfinance wanachaji kwa wananchi lakini pia na procedure mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tatizo ni kubwa, wananchi bado wanachajiwa riba kubwa na microfinance lakini pia hata ile procedure yenyewe, wanaweza wakapunguza bei ya kiasi cha riba lakini ile procedure ambayo ni application fee ni gharama kubwa kuliko hata riba yenyewe. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri suala la microfinance tuendelee kulifanyia kazi, kwa sababu huko ndiko wananchi wetu wengi wanapata mikopo kwa ajili ya biashara lakini pia na shughuli mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nilikuwa naangalia napitia bado tofauti kati ya bidhaa za kutoka nje hasa kwenye vinywaji, tofauti ya kodi kati ya bidhaa za kutoka nje na ndani ni ndogo sana. Hii bado naamini tunayo nafasi ya kufanya marekebisho kama ni kushusha kodi ya bidhaa za ndani au kupandisha ya nje, lengo ili tuweze kuwainda ipasavyo na kwa vitendo viwanda vya nchi yetu. Huwezi ukaweka tofauti labda ikawa ni 200 au 100 kwa lita halafu utegemee kwamba utapata matokeo ambayo ni mazuri sana, kwa hiyo, lazima hili liwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Nchi za wenzetu unakuta tofauti ni kubwa sana kiasi kwamba mtu akitaka kwenda kununua bidhaa ya nje kama ni kinywaji anafikiria mara mbili mara tatu kwa sababu bei inakua ni kubwa sana wakati mwingine inakuwa hata mara mbili ya kile cha nyumbani. Kwa hiyo, ni lazima tuliangalie tusiogope kufanya maamuzi kwa ajili ya kulinda viwanda vya ndani na ukiwabana sana hata hawa ambao wana viwanda nje hata vifaa tunapata kwa kodi kubwa wanakuja kujenga hapa hapa kwetu, wakija kujenga hapa maana yake sasa vijana wetu wanapata ajira, tunachukua kodi zaidi na tunapata wawekezaji kwa namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Wizara ya Fedha pia kutokana na utaraibu wake wa usimamizi wa stempu za kodi zile za ETS. Utaratibu huu umeendelea kuongeza kodi, umeendelea kuongeza kodi kwa nchi yetu lakini pia umeendelea kutupa taarifa hasa za uzalishaji maana wakati wa zamani wakati tunatumia zile stempu ambazo sio za kieletroniki kulikuwa na tatizo kubwa sana. Ilikuwa ni ngumu kuweza kujua kwa sababu forgery ilikuwa ni kubwa, ilikuwa ni ngumu kuweza kujua hasa uzalishaji ni kiasi gani lakini pia hata kodi ilikuwa ni ngumu kuweza kukusanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mnafanya kazi nzuri sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu hongera sana katika hili na usirudi nyuma wakati mwingine yanaweza yakaja manung’uniko yanaweza yakaja malamiko kwa sababu kama nilivyokuambia mkusanya kodi ni ngumu kuwa popular. Kwa hiyo, kanyaga na hata vetting mnayofanya kupata kampuni ambayo inafanya shughuli ile ya SICPA, mmefanya vizuri sana kwa sababu ni kampuni ambayo ukiangalia iko Dunia nzima. (Makofi)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, naomba utulivu ndani ya Bunge.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

TAARIFA

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi hapa Kingu niko…

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mchango mzuri sana unaotolewa na mchangiaji Kaka yangu Mheshimiwa Vuma, nilikuwa naomba nimpe taarifa kwamba pamoja na kwamba amesifia mpango mzuri wa stempu za eletroniki bado Serikali inaweza kuwa na nafasi ya kukaa na mzabuni wa SICPA kuona namna gani wanaweza wakapunguza bei, ambayo imekuwa ikionekana kidogo kwamba imeonekana kwamba ni changamoto ili kusudi Serikali ikaingia partnership na huyu mwekezaji ili Serikali iwe sehemu ya kumiliki teknolojia hii…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kingu hiyo ni taarifa au unachangia.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Naibu Spika, …na baada kuwasaidia Watanzania kupata teknolojia.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, napokea taarifa kwa mikono miwili, kwa nini? Kwa sababu nataka niseme, kabla hatuajanza mfumo huu Serikali imepoteza mapato mengi sana na nashauri tusiiishie tu hapo kwenye stempu hizi, tusiishie kwenye bidhaa ambazo zinatozwa kodi, hata bidhaa ambazo hazitozwi kodi nashauri tubandike stempu hizi ili tuweze kujua takwimu halisi kwamba tuna zalisha kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naunga mkono hoja na Mheshimiwa Dkt. Mwigulu usirudi nyuma kanyagia hapo hapo. Tunahitaji fedha kwa ajili ya maji majimboni, tunahitaji fedha kwa ajili ya vitu mbalimbali, tunahitaji fedha kwa ajili ya barabara vijijini. Endelea kukusanya kodi na hii kampuni kama alivyonipa taarifa Mheshimiwa Kingu ni vizuri tuendelee kushirikiana vizuri kwa sababu sio kila mtu anaweza kufanya kazi hii. Kuna kampuni chache ambazo zinaweza kufanya kazi hii. Kwa hiyo, tujitahidi tuwe makini, tusirudishe nyuma, kanyagia hapo hapo ili tuendelee kukusanya fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, liko suala la Benki ya Kilimo, Benki ya Kilimo hapa tumeshashauri mara nyini sana. Benki ya Kilimo ina stimulate sana uchumi wa nchi hii, kwa sababu ndio Benki ambayo inamjali mkulima kuliko benki yoyote ile huo ndio ukweli. Tumesema mara kadhaa hapa Mheshimiwa Dkt. Mwigulu tunaomba sana benki hii fanya consideration ya kuiongezea mtaji ili iweze kufikia Watanzania wengi Zaidi. Wananchi wengi huko hawapati mikopo ya Benki ya Kilimo kwa sababu mtaji ina maana ni mdogo. Kwa hiyo, tunaomba sana jitahidi sana uipe kipaumbele benki hii ya Tanzania ili iweze kuwafikia Watanzania ambao ni wengi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nilitaka kuzungumzia kuhusu maduka, utaratibu wa maduka ya kubadilisha fedha. Nadhani lazima tuangalie sheria ikoje inayo govern suala hili, kwa sababu utaratibu ni mgumu kiasi kwamba unalazimisha watu kufanya biashara hii katika namna ambayo sio halali. Yako maeneo hasa ya mpakani, maeneo ya mpakani hasa kama kule kwetu Kigoma na maeneo mengine, suala la kubadilisha dola ni suala la kila siku, watu wanatoka Congo, wanatoka Burundi, wanatoka Rwanda…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Vuma kengele ya pili.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja.

NAIBU SPIKA: Muda wako mwingi umetumia kwenye stempu.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kw Amuda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Sekunde tano.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana nishauri Serikali iweke utaratibu mzuri kwa kuruhusu biashara hii ifanyike vizuri waweze kupata kodi kupitia maduka ya kubadilishia fedha, nashukuru sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii na mimi kuchangia hoja hii ya Bajeti ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nipende kumpongeza Mheshimiwa Rais lakini na Waziri mwenyewe. Leo tarehe 01 Juni, waliahidi kwamba watashusha bei ya mafuta, kweli tumeona tangu jana usiku mafuta yameshuka imepunguza angalau makali ambayo yale ambayo Watanzania walikuwa wanayapata. Hongera sana Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwana nataka nizungumzie grid ya Taifa Mkoa wa Kigoma, ni matamanio ya wananchi wote wa Mkoa wa Kigoma kupata umeme wa uhakika kama ambavyo watanzania wengine wanapata. Kwa bahati mbaya sana hatujawahi kupata grid ya Taifa tangu tupate uhuru Mkoa wa Kigoma. Tumekuwa tunasema muda mrefu humu ndani na kwenye platform tofautitofauti lakini bado utekelezaji wake unasuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nimeona kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri, kwanza nishukuru kwamba kuna mawazo hayo ya kupeleka grid ya Taifa lakini nimeangalia figures bado is not convincing, ina maana huu mradi wa Urambo kwenda Kigoma ambao ni Bilioni 69.7 zimetengwa Bilioni 2.0. Nimeangalia huu wa Nyakanazi kwenda Kigoma ambao ni zaidi ya dola Milioni 35 ambao ni zaidi Bilioni 80 huko lakini tumetengewa Bilioni 7.4. Chondechonde Mheshimiwa Waziri unanisikia vizuri, wewe ni Kaka yangu, unajua hilo tunaheshimiana sana. Mkoa wa Kigoma tunaomba wakati tukiwa Waziri wa Nishati tuachie zawadi, tuachie legacy, Kigoma itakukumbuka wewe, itamkumbuka Mama Samia katika suala la umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza kusema mengi lakini mengi wewe unajua tumeshazungumza, nakuomba sana Kigoma tunataka grid ya Taifa, tumesubiri mno, Mikoa yote grid ya Taifa imeunganishwa bado Kigoma tu, kuna nini? Tunahitaji tutengewe fedha za kutosha siyo Bilioni Mbili hizi, tupewe fedha za kutosha ili miradi hii iende kwa kasi kubwa, ikamilike na wananchi waweze kupata grid ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la REA nashukuru vipo Vijiji ambavyo vimepata umeme lakini yapo maeneo makubwa hasa sisi Wabunge wa Vijiji, Kasulu Vijijini, kutokana na ile jiografia ya kule umbali wa kutoka Kijiji mpaka Kijiji yako maeneo mengi ambayo umeme kwa kweli haujafika. Ziko Kata kama saba Nyamwusi, Titie, Ungwempya, Kurugongo, ahsante Nyerere, Kitanga, Herushingo, Shunguriba hizi ni Kata kabisa ambazo umeme haujafika. Ningependa kasi ya kupeleka umeme Vijijini hasa Jimbo la Kasulu Vijijini yaongezeke kwa kasi kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la kukatikatika kwa umeme. Kama kuna jambo ambalo limekuwa linachafua Serikali ni la kukatikatika kwa umeme, tunaweza tukafanya mambo makubwa na mazuri sana lakini lazima tudhibiti jambo hili. Na nikupongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuja na mawazo haya ya kuimarisha grid ya Taifa. Umekuja kuomba Bilioni 500 hapa nimeona na Inshallah tutakupatia lakini nenda ukasimamie vizuri suala la kukatikakatika kwa umeme linachangia, linachafua mno Serikali kuliko kawaida. Umeme ukikatika tu watu wanatukanwa mno huko chini. Lazima tujitahidi sana hizi fedha ambazo utapatiwa uende ukafanye usimamizi mzuri sina mashaka na Mheshimiwa Waziri, naamini usimamizi utakuwa mzuri na hatimae suala la kukatikakatika umeme lilikuwa ni nchi nzima lakini sasa Kigoma lilikuwa ni balaa zaidi, ili kuhakikisha kwamba tunaweza kumaliza jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nataka nishauri jambo moja hii shilingi bilioni 500 nadhani kuna viwanda siku hizi vya kutengeneza vifaa mbalimbali vya umeme. Ningependa sana hii fedha sehemu kubwa ya fedha hii au chochote ambacho mnataka kununua ambacho kinapatikana hapa kwetu Tanzania vinunuliwe hapa hapa ili angalau kuweza kuongeza fedha kwenye mzunguko wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu ni hayo tu naunga mkono hoja all the best Mheshimiwa Waziri, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kukushukuru sana kwa nafasi hii nzuri ili na mimi niweze kuchangia Muswada huu wa upatikanaji wa taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naona ndugu yangu Heche alivyosikia jina langu limetajwa, baada yake alianza kutokwa na povu kama nimeandaliwa kwa ajili ya kumjibu. Niseme tu, mimi ni Mkristo safi, nitaendelea kusema ukweli, maana yake najua ukweli kwa mujibu wa dini yangu humweka mtu huru siku zote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais, alivyokuja kwenye kampeni Jimboni kwangu pale Kasulu aliahidi kwamba atafuta vumbi Wilayani Kasulu na juzi nimeenda kule kwenye ziara yangu ya kuwashukuru wananchi, nimekuta ujenzi wa barabara upo kwa kasi ya ajabu. Kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Rais. Nasema hayo kwa sababu wananchi waliniambia niseme. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, napenda kuishukuru Wizara ya Katiba na Sheria kwa Muswada huu. Muswada huu nimeupitia vizuri kuanzia kifungu cha kwanza mpaka kifungu cha mwisho cha 24. Nimeusoma vizuri lakini pia nimepata nafasi ya kupitia hii schedule of amendment to be moved na Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba mwandishi mmoja anaitwa Malisa, mwaka 2004 aliwahi kusema katika chapisho lake liitwalo Freedom of Information and Access to the Government Record Rose Around the World, alisema; “Access to information is the notion that public can obtain information and the possession of the state and in some countries private entities are information for the purpose of being informed about the activities of the state.”
Kwa tafsiri isiyo rasmi kwamba upatikanaji wa taarifa ni dhana ya kuwa Umma unaweza kupata taarifa zilizo chini ya himaya ya Serikali na katika baadhi ya nchi taasisi ya mtu binafsi kwa madhumuni…
Kwa madhumuni maalum, hiyo nimesema siyo rasmi.
Nataka niseme kwamba ni wakati sahihi kabisa Muswada huu umekuja, wazungu wanasema, information is power. Taarifa ni zao la habari, kama ikitolewa visivyo sahihi huzaa habari isiyo sahihi. Kama Taifa hatuna utaratibu, hatuna sheria ya upatikanji wa taarifa, maana yake inaweza ikatupelekea katika mazingira ambayo kila mtu hawezi kuamini. Maana yake taarifa hizi ambazo siyo sahihi zimesababisha baadhi ya Mataifa kuingia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe; vinapelekea baadhi ya usalama wa nchi mbalimbali duniani kupotea na kujikuta wakiwa katika mapigano na umwagaji wa damu. Kwahiyo, kuwa na sheria ya upatikanaji wa taarifa ni kitu sahihi kabisa na mimi naunga mkono Mheshimiwa Waziri mswada huu umekuja katika wakati sahihi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekaa nikafuatilia vizuri sana michango ya sehemu zote mbili; wapinzani na wengine lakini nimeona wengi tu hapa hasa ndugu zangu wa Upinzani wanarukia tu, hawajapata nafasi ya kuupitia vizuri muswada huu na wala hawajapata nafasi ya kupitia hii schedule of amendment. Kwa sababu naona ndugu yangu Mheshimiwa Heche pale na wengine waliosimama wakasema kwamba adhabu ni kali sana; lakini nikisoma kwenye schedule of amendment kipengele (c), ukija pale (a), (b), (c); kipengele cha (c) tena imeandikwa “by deleting sub clause and substituting for it the following; namba 6 (a):-
“Any person discloses exempted information other than information related to the national security commit an offence and shall on conviction be liable to imprisonment for the term not less than three years and not exceeding five years.” (Kicheko/Makofi)
Sasa nyie mnavyosema kwamba miaka 10 mpaka 15, maana yake mmerukia tu, mnataka kulidanganya Taifa; mmerukia bila kuangalia hii schedule of amendment.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, wamesema hata hapa kwamba sheria hii ipo Bara peke yake. Labda niseme kwamba sheria hii Uingereza ilitungwa mwaka 2002. Uingereza kule ilivyotungwa Scotland wao walikuwa hawakuitumia, kama sisi tunavyofanya hivi, wamekuja kuiingiza mwaka 2002. Kwa hiyo, tupo sahihi, tupitishe sheria hii bila mizengwe yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine wamekuja hapa wakasema kwamba hii sheria iondoke, yaani hawataki kufanya chochote. Sasa mimi nadhani tumekuja hapa tunalipwa na Watanzania. Tunalipwa mamilioni ya Watanzania kwa siku ili tupate nafasi ya kutunga sheria kama kazi yetu ya Kikatiba kama Wabunge. Sasa muswada umekuja hapa, badala tutoe michango ya kuuboresha na hatimaye iwe sheria nzuri na kurekebisha Tanzania, wewe unakuja unasema kwamba iondoke, yaani maana yake upokee hela tu pasipo kufanya kazi yoyote; hii ni akili kweli jamani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba ifike mahali tuwe wazalendo wa kutosha, tusizungumze tu hapa kwa sababu ya kutaka umaarufu, tusizungumze hapa tukaacha maslahi mapana ya nchi pembeni. Amekuja hapa ndugu yangu, mtani wangu, Mheshimiwa Lema jana kasema mshahara wa dhambi siku zote ni mauti, na mimi nasema, hayo ni maneno ya Kanisani, sisi hapa Bungeni tunasema kwamba mshahara wa kutoheshimu mamlaka ni kibano. Kwa mfano, umeambiwa ulipe kodi, halafu unakaa haulipi kodi, vyombo vyako tutatoa nje hata kama ni kiongozi mkubwa katika nchi hii. Umeambiwa Kanuni zinasema kwamba tutii Kiti hapa Bungeni, wewe hauachi kutii Kiti hapa Bungeni, wewe utatolewa hata kama ukifunga bandage mdomoni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu, naomba unilindie muda wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nasema hapa kwa sababu uzalendo wa watu, hasa ndugu zetu hawa umeondoka. Wamekuwa wakijaribu kutanguliza maslahi yao mbele pasi kutanguliza maslahi mapana ya Taifa. Wamekuja hapa Bunge lililopita, wamefungwa midomo na kiongozi wao wakaondoka, walivyoondoka kule wameshindwa kuona udikteta wa kiongozi wao…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu, tafadhali! Wameshindwa kuona udikteta wa kiongozi wao…
…wanakuja kutuambia kwamba Mheshimiwa Rais…
Mheshimiwa Mwenyekiti, tafadhali!
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu, tafadhali.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kuweka vizuri hali ya Bungeni. Niseme tu kwamba Muswada huu umekuja wakati sahihi na wote tuungane kwenye kuupitisha. Ahsante sana.