Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. David Mathayo David (5 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, napenda kuunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Pili, nawapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu kwa uongozi bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya mwaka 2013/2014 ilipitisha bajeti ya kuwapelekea huduma za mifugo (miundombinu) kama majosho, malambo na visima virefu. Pia mwaka 2015 wataalam wa Wizarani walitembelea Kata ya Ruvu na maeneo ya kujenga miundombinu hiyo. Je, miradi hiyo itakamilika lini na tutegemee miradi hiyo itaanza lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Nampongeza Mheshimiwa Waziri na Wizara yote kwa ujumla. Naomba kujua yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi mwisho wa mwaka wa fedha Mradi wa Maji Mwanga – Same utakuwa umefikia hatua gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa hali ya maji Mji wa Same, Makanya na Hedaru ni mbaya sana, je, Serikali itachimba lini visima virefu kabla ya mradi mkubwa wa maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Waziri, Waziri wa Fedha amesoma bajeti vizuri sana na nilikuwa namwangalia kwa makini hata maji alikuwa haombi na sauti yake imekwenda vizuri bila kupungua mpaka mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja, kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Spika, sababu ya kwanza, kwanza bajeti hii ni ya kihistoria, mimi nimekaa hapa miaka12 lakini ndio mara kwanza kusikia bajeti inayoeleweka kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Kwa hiyo ni bajeti ya kihistoria.

Mheshimiwa Spika, hii ni mara ya kwanza sera za viwanda, uanzishaji wa viwanda na ku-favour viwanda imejikita moja kwa moja kwenye bajeti ya Serikali. Bajeti hii imetoa majibu ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, bajeti hii vilevile inaonesha ni jinsi gani National Development Plan ilivyokuwa incorporated kwenye bajeti hii ya mwaka huu pamoja na dira ya Taifa ya mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bajeti hii pia imepunguzia wakulima na wafugaji ambao tunasema kwamba ni walala hoi wamepunguziwa kodi mbalimbali, hususani kwenye kilimo kwenye chakula kwenye madawa kwenye pembejeo mbalimbali, kwa hiyo ni bajeti ambayo inastahili kuungwa mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaeleze tu Waheshimiwa Wabunge ambao ni wapya kwa maana ya kwamba wameingia wale asilimia 70 kwamba wasishangae sana kupata kusikia Wapinzani wanaendelea kupinga bajeti hii. Hata siku moja Wapinzani hawajawahi kuunga mkono isipokuwa na kumbuka Mzee John Momose Cheyo na Mzee Augustino Lyatonga Mrema ndio walikuwa Wapinzani wa kweli na ndio waliokuwa wanasema ukweli, kama Mheshimiwa wa Chama cha CUF ambaye ndio amemaliza sasa hivi muda mchache uliopita kuongea. Ameongea vizuri kiungwana, lakini wenzetu pale hawakumpigia hata makofi kwa sababu alikuwa anaongea vitu vya ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kusema kwamba Wapinzani kazi yao ni kupinga na sisi kazi yetu ni kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa miaka mitano kwa sababu sisi ndio tulioshinda uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wapinzani hawa kwa wale wasiowajua ni watu ambao wanabadilikabadilika, wamekuwa ni kinyonga. Kwa mfano, mwaka 2015 wakati Mheshimiwa Lowassa yuko Chama cha Mapinduzi walikuwa wanasema ni fisadi, alivyohamia kwao wakampa kugombea Urais, sasa si wanabadilikabadilika hao. Sasa hivi tunazungumzia mikataba mbalimbali lakini wasisahau kwamba Mheshimiwa Sumaye ambaye alikuwa Waziri Mkuu kipindi hicho ndio alikuwa msimamizi wa shughuli za Serikali Bungeni alikuwa hapa wakati mikataba hiyo inaingiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii presha ambayo Wapinzani wanaiona ni kwa sababu wanajua kwamba 2020 tunapita bila kupingwa na viti vyao vitapungua.

TAARIFA ....

MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, siipokei taarifa hiyo kwa sababu akiwa kama Waziri Mkuu alitakiwa ahakikishe kwamba inatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ajenda ya Wapinzani kwa sasa walikuwa wanasema; maana sasa hivi wanasema kwamba bajeti hii ya Serikali haitekelezeki, lakini ajenda yao ya hapo nyuma, miezi miwili iliyopita walikuwa wanasema demokrasia imebanwa. Sasa hivi wamebadilika wanasema bajeti haitekelezeki, wakitoka hapo wataanza kusema tena demokrasia imebanwa, lakini embu waulize, sisi tangu

mwaka 2000 mpaka leo tumebadilisha Wenyeviti wa Chama cha Mapinduzi watatu, Mheshimiwa Mkapa, Mheshimiwa Kikwete na Mheshimiwa Magufuli, wao bado wako na Mbowe sijui mpaka miaka mingapi ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikimwona Tundu Lissu yeye ndio Mwenyekiti wa CHADEMA nitasema kweli mna demokrasia, lakini kama CHADEMA bado iko Moshi bado. (Makofi)

TAARIFA ....

Mheshimiwa Spika, Wapinzani wanasema kwamba Serikali itapata wapi trilioni 31.7 someni bajeti muone vyanzo vya mapato, kwa nini hamsomi?

Mheshimiwa Spika, kwanza Mheshimiwa Tundu Lissu akumbuke kwamba tulikuwa chama kimoja cha Chama cha Mapinduzi peke yake. Pili, kujikosoa siyo udhaifu bali ni dalili ya kujiendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shazia huwa inashona gunia, lakini shazia ili ishone gunia inatungwa uzi huku nyuma, sasa wasubiri 2020 tunawatunga uzi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ni kitu cha ajabu sana kuona kwamba Mheshimiwa Rais wetu, kwanza amefanya makubwa yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, nitayarudia tu halafu mtaona hamna hata mmoja atakayepiga makofi kule. Kwanza, ameondoa watumishi hewa zaidi ya 19,700. Pili, ameondoa watumishi wasio na vyeti 9,900; wanafunzi hewa walioondolewa kwenye Bodi ya Mikopo 3000; kugharamia elimu ya msingi hapo nyuma haikuwepo hii, elimu ya msingi sasa hivi inagharamiwa bila malipo, ukusanyaji wa kodi uliongezeka kuanzia bilioni 800 mpaka bilioni 1200 na zote hizo zinakwenda kwenye shughuli ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, pia ameweza kuhamishia Makao Makuu ya Serikali Dodoma, maamuzi haya yalifanyika mwaka 1973 lakini yamefanyika leo miezi 18 tayari Mheshimiwa Magufuli ameweza hiyo kazi. Ujenzi wa reli ya standard gauge haijawahi kutokea kwa muda mfupi namna hii. Kununua ndege mbili na zingine zinakuja na akina Mbowe ndio wanazipanda zinakuja, ni makubwa aliyofanya Mheshimiwa Jemedari wetu Dokta John Pombe Magufuli, kwa nini hampigi makofi? Hizi ndege mtapanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tumeshinda kwa kukubaliana na Uganda kujenga bomba refu kutoka Hoima mpaka Tanga, Wakenya nao walitaka lakini walishindwa kwa sababu tuko vizuri. Vilevile meli mbili zimenunuliwa kule Nyasa na wanazitumia wananchi na tumefanikiwa kuzuia makinikia kwenda nje na tumeshajua hela tuliyokuwa tunaibiwa. Mambo yote haya aliyoyafanya Mheshimiwa Rais anastahili hongera, anastahili kuombewa na viongozi, anastahili kuombewa na Wakristo na Waislamu ili aweze kuwa na afya na maisha marefu ili aendelee kutusaidia.

Mheshimiwa Spika, tunaomba kudhibiti kuwe na tracking system inayodhibiti magari yanayosafirisha mizigo, lakini kwenye ada ya registration kwa mara ya kwanza tunaomba angalau iongezeke laki moja kwa kila capacity ya engine kwa sababu hela iliyowekwa ya ongezeko la 50,000 ni hela ndogo sana, kwa sababu wana-register mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, hii ada ya magari iliyofutwa tunaomba ziongezeke Sh.50/= kwa kila lita ili tuweze kupeleka maji vijijini jamani, ndio maamuzi haya yatatusaidia.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii. Napenda pia kuwapongeza uongozi wa Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya wakisaidiana na watendaji wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri aliniahidi huduma ya umeme katika vijiji vyangu 50 vilivyobakia na ambavyo kampuni ya SPENCON ilishindwa kazi waliyopewa. Naomba kujua upelekaji wa umeme wa REA umefika wapi?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuzungumza machache kutokana na bajeti yetu hii. Nitazungumza masuala matatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza, bajeti ya kilimo ya mwaka huu kwanza ni ndogo. Kilimo kinachangia asilimia 85 ya kazi ambazo Watanzania wamejiajiri. Kilimo hiki kwenye pato la Taifa kinachangia asilimia 26.9 lakini kimetengewa kwenye bajeti asilimia 0.8. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba hizi shilingi milioni 500 kwa kila jimbo zitasaidia kutengeneza barabara za TARURA na hivyo kutoa mazao kwenye maeneo mbalimbali kupeleka kwenye soko. Kwa hiyo, hiyo nayo imechangia kwenye kilimo. Vilevile natambua kwamba tuna miradi mikubwa ya kimkakati ambayo inahitaji fedha nyingi, ndiyo maana pengine bajeti ya kilimo ni ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nashauri kwamba baada ya bajeti hii, kwa sababu hii tunaipitisha na imeshapita, ni kwamba mwaka kesho Waziri wa Fedha na Waziri wa Kilimo waweze kukaa mapema na kuangalia umuhimu wa kuendeleza sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja na kuimarisha skimu mbalimbali zile za umwagiliaji na kukarabati ambazo zipo. Tunahitaji takribani shilingi trilioni moja kwa miaka mitatu mfululizo kwa ajili ya kukarabati na kujenga skimu mbalimbali za umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tukumbuke na tukubali kwamba miundombinu ya umwagiliaji na miundombinu ya barabara zetu ni sawa kwa sababu food security inategemea kuwepo kwa chakula na chakula kile lazima kitokane na irrigation. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Hayati Benjamin Mkapa alitoa waraka kwamba District Cess ambayo inakusanywa kwenye Halmashauri, asilimia 20 irudi kwenye kilimo, lakini tumekaa muda mrefu, haijawahi kutekelezwa. Kwa hiyo, nilikuwa namwomba Mheshimiwa Waziri kipindi hiki iweze kuwekwa kwenye Finance Bill ili angalau asilimia 20 ya makusanyo yanayokusanywa kutokana na kodi ya mazao basi irudi kwenye kilimo kuliko kumkamua ng’ombe bila kumpa majani, anaweza akafa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nature ya kilimo inahusisha pia masuala ya utafiti ambapo tunatakiwa tutoe fedha mapema. Fedha zote hizi zikitoka, shilingi bilioni 294, basi itasaidia sana katika kuhakikisha kwamba tunaandaa masuala ya kilimo ambayo yanahitaji maandalizi ya haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili katika bajeti hii ambalo nilitaka nizungumzie ni sera ya fedha. Serikali kama ilivyo kawaida, haifanyi biashara, lakini BoT inawabana Watanzania. Inawabana wafanyabiashara kutoweza kufanya biashara kwa kutosha kabisa kupitia mabenki ya biashara. Wanabana namna gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kama nilivyosema, sekta binafsi ndiyo engine ya kuendeleza uchumi, lakini Benki Kuu inabana mabenki ya biashara kwa kusababisha ukwasi, matatizo ya ukwasi. Mabenki ya biashara hayana fedha za kukopesha wafanyabiashara na Watanzania ili waweze kufanyabiashara pamoja na kulipa kodi za Serikali. Sasa yanasababisha matatizo ya ukwasi namna gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzoni Serikali na taasisi zake zilikuwa zinaweka fedha zake kwenye mabenki ya biashara, lakini sasa hivi fedha zile zinalipwa moja kwa moja kwenye Benki Kuu ambapo mabenki ya biashara yanakosa fedha za kukopesha wafanyabiashara wadogo. La pili, hati fungani ambazo Serikali inakopa, inatoa riba kubwa sana kiasi ambacho mabenki ya biashara yanashindwa kufanya biashara ya fixed deposit. Kwa hiyo, watu wanakimbilia kwenye hati fungani kufanyabiashara na Serikali badala ya kufanya biashara na mabenki ya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuna riba kubwa sana ambapo wananchi na wafanyabiashara wanalipa mabenki ya biashara. Hii inatokana na kwamba Benki Kuu inapokopesha mabenki ya biashara inawatoza riba kubwa. Sasa hivi inawatoza asilimia 6.5 na mabenki ya biashara na yenyewe yanatoza asilimia 20; iwe ni mortgage au biashara nyingine yeyote, lakini ni asilimia 20. Sasa cha kufanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri yafuatayo: La kwanza uwekwe utaratibu ili Serikali iweze kupitishia fedha zake kwenye mabenki ya biashara kusudi kuwe na fedha za kutosha za kukopesha watu ili wafanye biashara na waweze kulipa kodi ili tuweze kufikia shilingi trilioni 22 ambazo tunatakiwa tuzilipe kupitia kwenye kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Benki Kuu ishushe riba zake inapokopesha mabenki ya biashara kusudi na mabenki yale yaweze kushusha riba yanapohudumia wafanyabiashara. Lingine ni kwamba, kwenye hizi hati fungani tunaomba kabisa Serikali kupitia Benki Kuu pia washushe riba angalau ifikie asilimia 10 kusudi mabenki yaweze kukopesha, kuchukua fedha za wafanyabiashara kwa fixed deposit na wenyewe angalau waweke asilimia kidogo. La sivyo tutakuwa tumeshaua kabisa kabisa, tutapunguza uchumi wetu. Kwa sababu sasa hivi kusema ukweli tuko kwenye middle income economy lakini tusipolinda uchumi huu, itafika pahala ambapo tunarudi kule kule kwenye umasikini mkubwa kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha aweze kuongea na mabenki ya biashara ili waweze kufungua matawi mbalimbali ya mabenki huko mikoani kwa sababu mabenki mengi yamefungua matawi mengi Dar es Salaam, Arusha, Mwanza na Moshi pamoja na Mbeya wakati mikoa mingine yote haina mabenki kama hayo. Hiyo ingesaidia kupunguza gharama kwa sababu wakopeshaji wangekuwa ni wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, sera za BoT ziangaliwe. Sasa hivi sera zilizopo ni za kunyanyapaa vijana. Vijana kila wanapotaka kukopa wanaambiwa uwe na nyumba, uwe na landed property. Sasa vijana wataweza wapi kupata landed property ili waweze kukopa? Kwa hiyo, hilo nalo liangaliwe kusudi vijana waweze kukopa na waweze kuendelea na biashara vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu, ningependa kuzungumza suala la Sera ya bajeti lakini kwa ushauri, bajeti hii ni nzuri na tunaipitisha kwa asilimia 100 lakini ningependa kushauri mambo machache yafuatavyo; jambo la kwanza suala lilikuwa linaathiri sana bajeti zetu ni matumizi ya dharula ambayo hayakupitishwa na Bunge, tunaiomba Serikali ijitahidi sana sana isiwe na matumizi ya dharura ambayo yanaathiri bajeti zetu ambazo zimetengwa na Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine ni kwamba labda tufanye utafiti kwa sababu nimeangalia hapa kuanzia mwaka 2005 mpaka leo kuna fedha zinazotengwa na Bunge na zile zinazotolewa kwenye mawizara inafikia tu asilimia 58 mpaka asilimia 67. Nadhani tuangalie inawezekana labda tuna over estimate bajeti zetu halafu tunashindwa kufikia malengo kutokana na uwezo wetu wa kukusanya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kwamba tunaomba Serikali iangalie athari za COVID au UVIKO-19 ili tuweze kusaidia baadhi ya biashara ambazo zimekuwa affected kwa mfano mabiashara ya mahotel ambayo pengine yangeweza kusamehewa baadhi ya kodi ili waweze kusimama kwa sababu wamekua affected sana sana na huu ugonjwa wa corona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuona faida ya miradi mikubwa ya kimkakati lazima tuhakikishe kwamba tunaimaliza mapema tuweze kuona faida yake na iweze kusaidia kujenga uchumi kupitia miradi mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwamba Serikali iweze kulipa ihakiki madeni ya ndani na iweze kuyalipa ili tuweze kuongeza mzunguko wa fedha na wananchi waweze kuendelea na biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi naunga mkono hoja.