Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Naghenjwa Livingstone Kaboyoka (41 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii maana nimeona mara nyingi hata nikileta maombi ya kuchangia sichaguliwi, lakini leo umenichagua ninakushukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kusema kwamba, kutokana na tamko la Kiongozi wetu wa Kambi ya Upinzani kuhusu uvunjaji wa Katiba ambao unawanyima wananchi wetu kufuatilia haya yanayotendeka hapa Bungeni ningeomba nisubiri mpaka tupate ufumbuzi wa tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiaw Mwenyekiti, kwanza niwapongeze wenzetu wa Kamati zote kwa kazi nzuri walizofanya. Najua ukiwa wa mwisho itakuwa point zako nyingi zimechukuliwa lakini nimebaki na chache ili nisirudie rudie zile ambazo wenzetu wamezisema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa tu nataka ni-observe mambo mawili, kwamba katika nchi yetu nafikiri tunatakiwa tuongeze uzalendo zaidi maana naona kwamba kila wakati tunasema tukaangalie wawekezaji kutoka huko nje. Hatuweki misingi ya kusema tujenge uwezo wa watu wetu wa ndani. Kama wenzangu waliotangulia waliosema Wachina, nakumbuka hata kile kisiwa cha Hong Kong wakati wazungu wale wa Uingereza wakitakiwa waondoke, 10 years before, waliwawezesha watu wao wawe na mitaji mikubwa waweze kuwekeza kwenye vie viwanda vikubwa na wawe board members ili waweze kujifunza na kupata uzoefu, ndiyo maana wenzetu mpaka leo China wamekwenda mbele sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwetu tunajua kwamba kuna aliyesema 50 percent ya mafuta yanaingizwa kutoka nje, infact ni 70 percent ya mafuta ya kula wakati alizeti zinalimwa sana na infact tungeongeza pressure au misaada kwa wakulima wetu wa zile alizeti tungehakikisha kwamba hatu-import mafuta ya kula. Wenzetu kutoka Kenya wanakuja kuchukua vitunguu hapo Singida wanavi-re-export, sisi tunabaki tunaangalia wakati vitunguu vinatoka kwetu. Tunadharau vitu vidogo vidogo, lakini tungeangalia bottom up tungejikuta tunasaidia wakulima zaidi as a result tukaboresha na umaskini tukauondoa katika level ile ya chini kwa kuweza kuunganisha viwanda vyetu na malighafi kutoka kwa wakulima wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tunaangalia institutions zetu, tuna TEMDO, CARMATEC, CBE, Dar Tech, Arusha Technical; wote hawa wanafanya kazi ambazo wangewekwa pamoja, wakasaidiwa, wangeweza ku-invent vitu vizuri na ushauri mzuri kwamba tu-invest kwenye nini na waweze kuweka utaalam wao pale. Hivi vyote vimewekwa pembeni tunaangalia watu wa nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mabalozi wetu wametumwa nje, wanaambiwa muangaie wawekezaji, samahani sikumbuki labda imesemwa hiyo; lakini ningetegema nchi iwe ime-identify ni mazao gani tunaweza ku-export ili kila Balozi anayekwenda nchi fulani tumwambie atuangalilie soko la kitu hiki na kile na kile. For example, vitu vinavyolimwa Tanzania ambavyo tunaweza kupeleka nje ni vitu kama nini? Tunaweza kusema ni mzaha mzaha lakini tangawizi ambayo tunaweza kuiboresha, ni nchi yetu ina-produce tangawizi the best katika Afrika, lakini hivyo vyote hatuviangalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaangalia maziwa tuna-import mengi, kwa nini hatuboreshi viwanda vyetu watu wakasaidiwa, wafugaji wakazalisha maziwa kuliko ku-import maziwa, viwanda vile vikakuzwa. Unaona kuna ASAS Iringa, kuna kiwanda cha maziwa cha Tanga hatutaki kuviboresha badala yake tuna-import maziwa ya unga, yanakuwa imported sijui madawa gani kutoka South America yanakuwa packed, tunapata maziwa ya hovyo hovyo. Sasa kuna mambo mengi sana, kwamba bado uzalendo wetu haupo kuangalia kwamba tukuze from the bottom up halafu tuwe na inward looking badala ya kila siku tunasema kalete wawekezaji, wawekezaji ambao wakija wanatunyanyasa. Tunajua kuna viwanda watu wamewaweka huko hawajui hata Kiswahili sasa ndiyo tunayoyataka hayo. Mimi nafikiri ifike high time ambayo tutaweza kuangalia kwamba tunasaidiaje watu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie suala la mitaji, banks zinaweka riba kubwa sana kwa nini tusiwe na strategic plan ya kuona kwamba tuna-identify viwanda gani ambavyo tuwaboreshe watu wetu na tuwape…….
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuunga mkono mapendekezo ya Kamati hii, naomba kusisitiza kwamba migogoro ya ardhi hasa vijijini imezidi kuongezeka siku hadi siku. Kutopimwa ardhi kumesababisha miingiliano na vurugu kubwa hasa ikizingatiwa kwamba maeneo mengi ya vijijini hayajapangiwa matumizi bora ya ardhi zao, kwa mfano, Jimboni kwangu Same Mashariki, wakulima na wafugaji na TANAPA (Mkomazi National Park).

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wa wanyamapori kuingia kwenye mashamba na makazi ya wananchi umeongeza umaskini Jimboni kwangu. Mazao ya wakulima yamekuwa yakiharibiwa sana na wanyamapori. Wananchi wengine wameumizwa na wanyama hao. Badala ya kulipwa fidia, wananchi wamekuwa wakipewa kifuta jasho ambacho sio sawa na madhara waliyopata. Wanyamapori wamekuwa wakithaminiwa kuliko wananchi. Matokeo yake wananchi hawaoni faida ya kuwa na mbuga za wanyama katika maeneo yao. Nashauri Wizara hii ya Maliasili na Utalii ikishirikiana na Wizara ya Ardhi iweke utaratibu mzuri utakaoondoa matatizo haya ya wananchi.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika na Bunge lako Tukufu, nishukuru kupata tena nafasi hii kuweza kuhitimisha hoja hii ambayo imeleta sijui niite malumbano au utata mkubwa sana au mjadala mkubwa ndiyo Kiswahili hicho, mimi Mpare kwa hiyo Kiswahili wakati mwingine inakuwa shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, muhtasari wa kuhitimisha hoja ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC). Naomba kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja ya Kamati, jumla yao walikuwa Wabunge kama 11 waliochangia kwa kuzungumza hapa ndani ya Bunge. Sijapata michango yoyote kwa maandishi na nadhani labda haipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa ufafanuzi kwa baadhi ya hoja zilizotolewa na wajumbe ambazo kwa ujumla wake zote zimelenga kuboresha usimamizi wa fedha za umma katika Serikali Kuu na Mashirika ya Umma. Nikianza na wenzangu tuliokuwa nao kwenye Kamati na kutengeneza ripoti hii Mheshimiwa Kiswaga amezungumzia kuhusu miradi ya NSSF na viashiria vya ubadhirifu katika miradi hiyo. Nakubaliana naye ni muhimu kwa Serikali kufanya uchunguzi wa kina kwa watu wote waliohusika na manunuzi haya ya ardhi na kuchukua hatua stahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kiula ameongelea suala la tofauti ya shilingi trilioni 1.5 na kubainisha kuwa ni kweli kulikuwa na changamoto za takwimu katika suala hilo wakati ukaguzi unakamilika. Kama mapendekezo ya Kamati yalivyofafanua, tumependekeza kuongeza nguvu zaidi katika utunzaji wa kumbukumbu na wafanyakazi wenye weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ameongelea suala la mikopo ya matrekta ya SUMA JKT. Kamati inasisitiza kuwa madeni haya yalipwe na viongozi wa Serikali waliokopa matrekta hayo waonyeshe mfano kwa kulipa madeni hayo kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ali Salim ameongelea kuhusu kuboreshwa kwa mfumo wa Hazina wa utunzaji wa taarifa za hesabu. Amesisitiza kuwa uhamisho wa fedha ufanyike kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Stanslaus Mabula ameongelea kuhusu suala la uwezo wa kibajeti wa CAG. Ni kweli kwa mwaka huu CAG amefanikiwa kukamilisha kazi ya ukaguzi wa wakati. Aidha, amesisitiza kuwa watuhumiwa wa suala la malipo ya ration kwa watu wasiokuwa askari ni lazima wahusika wafikishwe kwenye vyombo vya sheria haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Zitto Kabwe aliongelea kuhusu suala la over released funds from the Consolidated Fund to some votes. Naomba kufafanua tu suala hilo kwa ufupi, kufuatia mabadiliko ya mzunguko wa bajeti hapo awali, uhamisho wa bajeti uliandaliwa baada ya kufungwa mwaka wa fedha na kuletwa Bungeni wakati Bunge likiendelea hadi mwezi Agosti. Baada ya mzunguko wa bajeti kubadilika, taarifa za uhamisho wa bajeti zimekuwa zikiandaliwa mapema ili kuwasilishwa kabla ya mkutano wa bajeti kukamilika tarehe 30 Juni kila mwaka. Hivyo Hazina imekuwa ikisitisha maombi ya uhamisho wa fedha kila ifikapo tarehe 15 Juni ya kila mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, panapokuwa na mahitaji maalum baada ya tarehe hiyo, maombi hayo hupokelewa na taarifa yake hutolewa katika taarifa ya mwisho wa mwaka. Kwa kuzingatia Sheria ya Bajeti ya mwaka 2015 na mzunguko mpana wa bajeti, taarifa za uhamisho wa fedha hutolewa kila baada ya utekelezaji wa bajeti wa kipindi cha nusu mwaka. Kutokana na majibu hayo, baada ya uhakiki wa CAG kukamilika, hapakuwa na fedha zaidi ya bajeti iliyoidhinishwa kwenye mafungu husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Felister Bura amesisitiza kuhusu tofauti iliyokuwa imejitokeza hapo awali kwenye tofauti ya makusanyo na fedha zilizotolewa. Nakubaliana naye kuwa ni muhimu Serikali ikaendelea kuchukua hatua kwa watu ambao wanahusika na miradi isiyokuwa na tija. Ametolea mfano hatua zilizochukuliwa NSSF kwa Wakurugenzi waliokuwepo hapo awali. Kamati inaendelea kusisitiza kuwa ni muhimu hatua zaidi zikachukuliwa NSSF hasa kwenye suala la miradi ya ununuzi ya ardhi ambayo imeonyesha kutokuwa na tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Khadija Nassir amezungumza kuhusu ushauri ambao umekuwa ukitolewa na Kamati. Katika hili nipenda kuishauri Serikali kutekeleza ushauri wa Kamati na Maazimio ya Bunge kwa wakati. Haipendezi Maazimio ya Bunge kutolewa kwa zaidi ya mwaka mmoja bila ya kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Anatropia ameongelea suala la uweledi wa watumishi katika Wizara ya Fedha na Mipango. Jambo hili tumelilisitiza kuwa ni muhimu likaangaliwa kwa makini, ni sahihi kuwa maboresho ya mifumo iliyopo Hazina ni lazima iendane na kuongeza weledi wa watumishi ili kumbukumbu za Mfuko Mkuu ziwe sahihi na Mheshimiwa Omari Kigua amejaribu tu kufafanua kwamba kumekuwa na mikanganyo ya kutumia MS Excel pamoja mifumo mingine. Hata hivyo ni kweli CAG aligusia kwamba kuna taarifa ambazo zilitengenezwa kwa kutumia excel na kwa ajili hiyo ndiyo maana hata kwenye Kamati kulikuwa na hoja kwamba je hizi taarifa nyingine ambazo zilitumika kwa kutumia excel ni za kuaminika?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mara nyingine tena namshukuru Mheshimiwa Spika kwa uongozi wake dhabiti nakushukuru pia wewe binafsi kwa uongozi wa Bunge letu, nawashukuru wajumbe wenzangu wa Kamati kwa ushirikiano wao mkubwa hadi kukamilika kwa taarifa hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumaini yetu kuwa Serikali itazingatia kwa ukamilifu uchambuzi wa Kamati na kutekeleza mapendekezo ya Kamati. Nipende kuchukua nafasi hii kusema kwamba Bunge lako limeshuhudia mapendekezo yalitolewa mara ya mwisho mwaka jana kipindi kama hiki manne yote ambayo ni muhimu sana hayajafanyiwa kazi. Sasa hapo ni wazi kwamba wale wahusika wote ni kama wamedharau Bunge, maana wasingekuwa wamelidharau Bunge wangeweza kuleta angalau taaarifa ya kuonyesha kwamba wamefikia wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nipende kusema kwamba hapa kumetokea majadiliano mazito kutokana na fedha hii ya trilioni 1.5, kwa mtu aliyeko nje ni rahisi aone kwamba kuna kitu kinafichwa katika hela hii. Pamoja na kwamba tumesikia pande zote zinazosema kuna tatizo na zile zinazosema hazina tatizo, nipende kusema kwa kipindi kinachokuja wakati CAG atakapofanya ukaguzi ni vyema akapitia kwa undani suala hili pamoja na matatizo mengine ambayo yametokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili kwa nini? Ni kwa sababu kwanza hii halikuja kama hoja haikuwa imekuja kama hoja kwa hiyo hata sisi kwenye Kamati tulipata shida sana kwamba tunalibebaje wakati halikujaa kama hoja. Lakini sasa tunaona muda mwingi Bunge limechukua katika kuzungumzia hili trilioni 1.5 kwa maana hiyo ni kwamba hata Mheshimiwa Rais unakumbuka mwaka jana alimuuliza CAG kwamba je, hii hela imeibiwa? Na akaendelea kusema kama ingekuwa imeibiwa ningechukua hatua kali sana kwa wahusika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naamini Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli huko aliko akisikia hii mijadala lazima aingie na mashaka kwamba kulikoni nitaangalia vile vifungu vyote vya taarifa yetu ambavyo vimeonesha kwamba Hazina walikubali kwamba kuna sehemu ambayo wamekosea wakakiri. Kwa maana hiyo ni kwamba kuna maeneo ambayo hayajatendewa haki. (Makofi)

Kama ukiongelea masuala yaliyoleta utata limetokana na mfumo swali ambalo Waheshimiwa Wabunge wengi ambao wanaweza kujiuliza wa pande zote mbili kama mfumo una matatizo je, taarifa zilizokuja inawezekana zisiwe na matatizo? (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo unapoongelea mfumo unaongelea kwamba huo mfumo na CAG amesisitiza hata sisi kwenye Kamati tumezungumzia mifumo unaweza ukatupa taarifa zisizo sahihi, ndiyo maana nasema CAG atakapofanya ukaguzi kipindi kinachokuja na kwa vile Hazina wamesema wanaweka mfumo bora basi atuletee taarifa maalum ya kuonesha kwamba mifumo imekaaje na je, mfumo wa awali umetuleta taarifa sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu weledi wa CAG amezungumza kwa urefu sana jinsi ambavyo alipata taarifa kwa shida ukiangalia taarifa inaonyesha akitaka taarifa hii inachukua muda sansa kupata majibu, wale wafanyakazi watakwenda huko watakaa muda mrefu bila kuleta taarifa kwa wakati, kwa maana hiyo hii ina maana gani ni kwamba Hazina haijawa-well organized, ama wafanyakazi lingine wanaloweza kufanya pia by profession ni administrator ni kwamba kunawezekana kuna wafanyakazi wengi wapya ambao hawakufanyiwa mafunzo ya kuweza kuweka taarifa vizuri kiasi kwamba ukitafuta taarifa huipati. (Makofi)

Kwa hiyo ndiyo maana pamoja na kwamba Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kweli kuna wabobezi kwenye mahesabu, lakini pia ikubalike kwamba kama hakuna utaratibu mzuri wa kuweka taarifa haiwezi kuleta tija katika sehemu kubwa au katika jicho la nchi ya Wizara ya Fedha na Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo ndiyo tulisema hata wakati itakapofanyiwa ukaguzi tutahitaji CAG atueleze kuhusu utata huu wa kutopata taarifa kwa wakati aliohuitaji kwamba alichukua muda mrefu katika hii verification kupata documents imetokana na nini? Je, ni uzembe ule ule wa kimfumo? Je, ni uzembe wa wafanyakazi? Je, ni kwamba hapakuwa na mafunzo ya kuelimisha wale wapya walioingia jinsi ya kuweka taarifa hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo twende kusema kwamba hapa wote tukubali maana siye tunaongea kama Bunge na wananchi wanatusikiliza sana na hatupo katika ushabiki wa vyama, na mimi kama Mwenyekiti wa PAC nipende kusema tunapenda popote walipo wananchi wetu waelewe kwamba Bunge liko serious kutokana na haya ambayo yanateandeka au ambayo yameonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo tusichukulie kisiasa tukazungumzia juu juu kwamba suala hili limefungwa lazima tunapoona suala limeleta utata mkubwa tuangalie kwanza aulize kwa nini hapakuwa na hoja ya CAG ili verification hii ambayo imefanywa na mfumo au mifumo ambayo ina utata je imeleta taarifa sahihi? Kwa hiyo nipende kusema kwamba naomba Bunge lako likubali kwamba wakati CAG atakapofanya ukaguzi unaokuja atuangalizie haya masuala ambayo yamefikisha Bunge lako kuwa na discussion kubwa kwenye trilioni 1.5 ambayo kwanza haikuwa hoja, lakini mfumo na weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona matatizo mengi ya fedha ambayo yamechukuliwa kwenye mashirika ambayo tungechukua muda mwingi pia kuangalia hao wote waliochukua fedha nyingi hivyo na bado wapo wengine kwenye kazi, hao waliochukua mikopo ambao bado wapo Serikalini na ambao wamestaafu. Imekuwaje kuwe na kigugumizi cha kuchukua hatua stahiki, kwa nini Benki ambazo zinatumia fedha za umma waoe kigugumizi kuchukulia watu hatua ambao ni wadaiwa sugu wakati benki zetu nyingine za biashara hawatoi mwanya kama huo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nategemea Bunge lako lizamie katika sehemu hii ambapo kuna pesa nyingi inapotea na ujue kwamba hii ripoti iliyokuja ni ndogo tu ya sehemu kubwa ya tatizo kubwa ambalo tungekwenda maradi hadi mradi kuanzia NSSF na mashirika yote mngeona matrilion ambayo yamepotea. Kwa hiyo, tusingezungumzia tena trilioni 1.5 kwa uzito huo ukilinganilisha na hizi zinazopotea katika miradi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe kwamba Bunge lako lijalo kama ni semina tupatiwe semina ya kwamba hizi taarifa tunazichambuaje kwa uweledi tutakapokwenda kivyama tutapoteza mwelekeo na utashi wa Bunge hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme kwamba baada ya maelezo hayo naomba kutoa hoja sasa kwamba Bunge likubali mapendekezo ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali PAC ili yawe Maazimio ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru tena kwa mara nyingine kwa kunipa nafasi ya kuhitimisha hoja hii muhimu ya Kamati. Naomba kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja ya Kamati na pia naomba kutoa ufafanuzi na maelezo ya
msisitizo kwa baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kuhusu utaratibu wa utekelezaji wa kazi za PAC, Kamati ya PAC inafanya kazi kwa mujibu wa Kanuni za Bunge. Hoja zilizowasilishwa na Kamati katika taarifa hii ni zile tu ambazo Maafisa Masuuli husika walihojiwa na Kamati na majibu ya hoja zao kufanyiwa uhakiki yaani verification na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hoja ambazo hazikufanyiwa uhakiki na CAG na Maafisa Masuuli husika kutohojiwa hazikujumuishwa katika Taarifa hii. Kwa muhtasari hoja zote za Waheshimiwa Wabunge zimesisitiza utekelezaji wa mapendekezo ya Kamati katika maeneo mahsusi ili kuboresha usimamizi wa fedha za umma katika Serikali Kuu na Mashirika ya Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapitio ya baadhi ya hoja hizo ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Allan Kiula amechangia kuhusu hoja ya ukusanyaji wa mapato inayotekelezwa na TRA. Amesisitiza kuwa TRA ni roho ya Taifa, hivyo, lazima TRA ifanyie kazi changamoto kadhaa ili kodi zote ziweze kukusanywa kwa wakati. Ni vyema hoja na pendekezo la Kamati linalohusu weledi na ufanisi likazingatiwa. Aidha, kesi za kodi ni muhimu zikamalizika kwa wakati na zile kodi ambazo hazikusanyiki ni vema zifutwe ili vitabu vya hesabu za TRA ziwe sahihi. Aidha, Mheshimiwa Kiula amesisitiza pia kuhusu kukwama kwa Miradi ya TBA na NHC na hivyo mapendekezo ya Kamati kuhusu kukamilisha Miradi ya Taasisi hizi ni vyema yakazingatiwa ili kuokoa fedha za Serikali;

Mheshimiwa Ali Salim khamis ameongelea suala la kutokamilika kwa usimikaji wa mifumo ya usimamizi na udhibiti wa shughuli za Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA). Amebainisha namna ambayo Viongozi wetu Wakuu wa Nchi wamekuwa wakisisitiza kuhusu suala la mapato ya Bandari, hivyo anasisitiza TPA ikamilishe Usimikaji huo mapema ili kudhibiti mapato ya Serikali;

Mheshimiwa Felister Bura amebainisha kuhusu gharama zinazoongezeka kwa Miradi ya NHC iliyosimama kwa muda mrefu kutokana na Wakandarasi kuendelea kuwepo eneo la Mradi. Kama Waheshimiwa Wabunge walivyochangia mawazo, naye pia anasisitiza kutekelezwa kwa mapendekezo ya Kamati ya kuangalia namna bora ya kukamilisha Miradi hiyo ili kuokoa fedha za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimimiwa Anatropia Theonest, mchangiaji wa nne pamoja na mambo mengine amesisitiza kuhusu umuhimu wa TRA kuendelea kuongeza ufanisi ili kufikia lengo la ukusanyaji wa mapato ya Serikali. Kamati inaamini mapendekezo ya Bunge yatazingatiwa na mwaka ujao wa fedha TRA itavuka malengo ya ukusanyaji kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Joyce Sokombi amechangia kuhusu ucheleweshaji wa Miradi ya TBA kwa sababu mbalimbali kama usimamizi mbovu wa Miradi na uhamishaji wa vifaa katika miradi. Ametoa mfano wa Jengo la Tume ya Uchaguzi Dodoma, hivyo ni muhimu mapendekezo ya Kamati kuhua TBA yakafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Kigua amelifahamisha Bunge kuhusu kupungua kwa hoja za Ukaguzi ikilinganishwa na miaka ya nyuma. Namshukuru pia Mheshimiwa Kigua kwa kutoa ufafanuzi kuhusu namna Kamati inavyoshughulikia hoja za Ukaguzi baada ya uhakiki wa CAG. Aidha, amesisitiza kuhusu umuhimu wa ukadiriaji sahihi wa kodi na kumalizika kwa kesi zaidi ya mia nane za kodi, amesisitiza kuhusu pia NHIF na NHC. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mambo mawili ambayo yamejitokeza ambayo nafikiri Kamati ni vyema tukayazungumzia, pamoja na kwamba tunasema kwamba mambo haya hayako kwenye, maeneo haya hayako kwenye Kamati yetu katika Taarifa hii, ni vyema mimi nikiwa Mwenyekiti wa PAC kwa vile yametajwa na kwa vile Rais wetu wa Nchi, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ametajwa kuhusiana na kumwajibisha Mheshimiwa Kangi Lugola ni vizuri pia nikataja mambo ambayo nafikiri kwamba yataweza kumfanya Rais Dkt. John Pombe Magufuli asionekane ni mtu wa double standard (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Anatropia alisema kwamba kama Mheshimiwa Kangi Lugola alitolewa katika nafasi yake kutokana na kutoleta Mikataba ya Zimamoto hapa Bungeni, yeye alitoa wasiwasi kwamba kuna Mikataba ambayo imeonekana haikuletwa hapa na ikafanya Kamati ishindwe kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninachosema kama Mwenyekiti wa PAC ni kwamba, kwanza kuna Mkataba huu wa E-Migration, huu Mkataba Kamati ilikaa na ikaomba Serikali ilete ule Mkataba ili uweze kuufanyia kazi. Badala ya Afisa Masuuli kujibu au kuleta tukapata maelezo ambayo barua ninayo sina haja ya kusema details kwamba Kamati tulimalize tu maana lina mambo nyeti, kitu kilichonishangaza uandishi wa maelekezo haya hauonyeshi kwamba una weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza mwandishi huyu hakuweza kuelewa kwamba Kamati ya PAC inafanya kazi kutokana na taratibu zilizowekwa na Bunge hili Tukufu, Kamati haina Mamlaka kufuta hoja yoyote ya CAG kama hoja ile haikuletewa vielelezo au kama CAG hakuelewa au hakukubaliana na yale maelezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo nilichukua hatua ya kuongea na Spika na kumwambia Mheshimiwa Spika, kazi uliyotupa PAC ni kufuata taratibu za Bunge, taratibu zilizowekwa na Bunge kwamba hela yoyote ya Serikali ambayo imetolewa lazima itolewe maelezo kwamba imetumikaje. Kutokana na huu mfumo wa E-Migration, kilichotakiwa siyo kuangalia kama kuna coding au kuna nini nyeti za ule mfumo, kilichotakiwa ni jinsi manunuzi yalivyofanyika kama Sheria ya Manunuzi imefuatwa, pesa zimelipwa ilivyotakiwa na ni kiasi gani ili kusudi hata mapato yanayotokana na hizi passports ionyeshe kwamba inawiana na investment iliyofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikasema kama Mwenyekiti kwamba, inaelekea Rais hakushauriwa vizuri maana Rais angeshauriwa vizuri ingekuwa ifuatwe taratibu iliyowekwa na Bunge na ndiyo maana Rais alivyogundua yaliyotokea kwa Mheshimiwa Kangi Lugola alimsimamisha akamwajibisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama hivyo ndivyo tunategemea hata hili la E-Migration halijakwisha, bado tutalifanyia kazi pamoja na CAG na kuona kwamba utaratibu unafuatwa na kama kuna jambo lolote tunategemea Rais akae na Spika, ili amweleze tatizo ni nini, Spika aweze kumshauri kutokana na Sheria za Kibunge ili kuanzia hapo sisi na CAG Kamati ya PAC ndiyo tunaweza kukaa na kusema hili jambo limefungwa au bado. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala lingine ambalo mimi nilihusishwa na Kamati yangu, wachache wetu kuhusu uniform za Polisi, kuhusu uniform za Polisi maana tunataka kumtoa Rais wetu asionekane ana double standard, mimi nilikuwa nimesafiri, nilikuwa South Africa nikapata barua kwamba wenzangu wameteuliwa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na wachache wa Kamati yangu kwenda kuangalia zile uniform za Polisi, wakati huo alikuwa Mheshimiwa Zungu ndiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikamwambia Mheshimiwa Zungu naenda kama nani kwa vile, mimi kama naenda kukagua na Kamati yangu, ina maana tumekaa na CAG tumepitia zile nyaraka zote zilizotakiwa maana suala la CAG halikuwa kwamba uniform tukazione kwa macho. Suala la CAG ilikuwa tuangalie namna uniform zile zilivyonunuliwa; je, huyo aliyepewa tender alipatikanaje? Uniform zililetwa kutoka wapi? Ziliingia bills of laiding ziliingia vipi, zikoje, kiasi cha fedha iliyotumika ni ngapi, from there ndiyo CAG aweze kwenda store kuangalia kuna nini? Kutokana na zile ripoti aone kwamba hizi uniform ziliagizwa 100, zimekuja 100, viatu viliagizwa 10 vimekuja 10? Kinyume cha hapo CAG hawezi kutoka akaenda kwenye store akaangalia kitu ambacho hana documentation kwamba anaangalia nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kulikuwa na mis-conception ambayo Mheshimiwa Kangi Lugola ali miss-lead Bunge kwa kuapa na kusema atavua nguo kama uniform hazipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ina maana hasomi hata taratibu za kwamba...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ngoja tuongozane vizuri.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa.

NAIBU SPIKA: Wewe hapo sasa hivi unavyozungumza ni kana kwamba nawe ni mchangiaji wewe ni mtu ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ambaye umekasimiwa madaraka ili uje ujibu hoja za Wabunge na humpi mtu mwingine hoja na baada ya kuzungumza wewe, maazimio uliyotuletea Bunge litahojiwa.

Sasa kama unatupeleka kwenye hoja tena nyingine na wewe ndiye uliyeleta taarifa hapa ndani Mwenyekiti utakuwa unaliongoza Bunge sehemu siyo. Kwa sababu wewe unapaswa kuzijibu hoja za Wabunge na siyo kuuliza kwa sababu hakuna mtu wa kukujibu, Serikali kwenye hoja hii wao ni wachangiaji kama mchangiaji mwingine, sasa ukija na wewe unauliza maswali, sasa nani atakayekujibu hayo maswali na wewe hii ndiyo hoja yako wewe. Hii ni hoja Mwenyekiti, kwa hiyo hoja zote zilizoletwa na Wabunge wewe ndiyo unazijibu hapo siyo mtu mwingine.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa. Nakushukuru.

NAIBU SPIKA: Ngoja tuongozane vizuri, kama kuna hoja ambazo kwenye Kamati hamkuzimaliza hilo ni la kwako Mwenyekiti, Serikali haiwezi kujibu hapa.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawasawa.

NAIBU SPIKA: Wewe ndiyo unayejibu hoja zote zilizotolewa na hata hayo maswali unayouliza nilikuwa nataka tu nione unaelekea wapi.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa.

NAIBU SPIKA: Hata maswali unayouliza yote ni ya kwako wewe utujibu hapa kama Bunge ili tuweze kuamua kwenye Maazimio uliyoyaleta wewe na Kamati yako.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa muongozo wako na hapo ndiyo nilikuwa nafikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili nitalitaja huko kwamba bado hili tutalifanyia kazi, kwa hiyo, umenieleza vizuri sana na nimekuelewa. Nataka nisahihishe kwamba…

NAIBU SPIKA: Mwenyekiti samahani, nisikilize kidogo.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo naendelea na hoja.

NAIBU SPIKA: Kwenye maazimio ya kwenye kitabu chako hiki hayo unayotaka kuyaleta, sina hapa mezani mabadiliko yoyote kwenye taarifa hii.

(Hapa baadhi Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge tufuate Kanuni zetu, kama unataka kuleta mabadiliko kwenye Maazimio lazima mimi niwe nayo hapa mezani ni wapi unabadilisha na hayo mimi sina, kwa hivyo Mwenyekiti huwezi kutoa ahadi hapo ukataraji tutalihoji Bunge kwenye hizo ahadi, hapana, siyo utaratibu kikanuni.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuelewa. Ni kwa vile…

NAIBU SPIKA: Kwa hiyo wewe jibu hoja za Wabunge walizokuletea, huwezi kuanzisha hoja mpya ili Bunge lihojiwe, Bunge litahojiwa kwenye taarifa uliyoleta na Maazimio uliyoyaleta.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa nakuelewa sana na nakushukuru, nilitaka nitoe tu ile kwamba Rais asionekane ana double standard.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mwongozo wako…

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, maana kuna mambo ambayo inawezekana hakupelekewa ndiyo nilitaka tu kueleza hivyo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, Mwongozo tu kidogo.

MBUNGE FULANI: …asituletee mambo yenu hapa…

NAIBU SPIKA: Hamna Mwongozo akiwa mtu anazungumza, wewe unajua Kanuni na nitakuruhusu uisome hapo umesema mwongozo hakuna mwongozo mtu akiwa anazungumza, naomba ukae.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu…

NAIBU SPIKA: Naomba ukae, naomba ukae…

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu…

NAIBU SPIKA: Naomba ukae Mheshimiwa Halima. Naomba ukae. Mheshimiwa Kaboyoka.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, Kuhusu Utaratibu…

MBUNGE FULANI: Nyamaza…

(Hapa baadhi Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipende kumpongeza Mheshimiwa Waziri Biteko kwa jinsi alivyoeleza kuhusu STAMICO na hatua ambazo amezichukua pamoja na Waziri wa Fedha. Kwa hiyo, nasema kwamba pamoja na maelezo yao ambayo ni mazuri na nawashukuru kwamba wameonyesha picha halisi hasa Mheshimiwa Biteko ambaye ameonesha jinsi ambavyo STAMICO imeshughulikiwa bado tutahitaji kupata verification kutoka kwa CAG. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nahitimisha kwa kumshukuru Mheshimiwa Spika kwa uongozi wake thabiti, nakushukuru pia wewe binafsi kwa uongozi wa Bunge letu, nawashukuru Wajumbe wenzangu wa Kamati kwa ushirikiano wao mkubwa hadi kukamilika kwa taarifa hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumaini yetu kuwa Serikali itazingatia kwa ukamilifu uchambuzi wa Kamati na kutekeleza mapendekezo ya Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na nawashukuru pia Wabunge wote kwa kunisikiliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, naomba kutoka hoja kwamba Bunge lako sasa lipokee na kukubali taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali PAC kuhusu shughuli za Kamati hiyo kwa mwaka 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa jina naitwa Naghenjwa au wale waliozoea wananiita Naghe Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupatiwa nafasi hii kutoa mawazo au maoni yangu machache kutokana na hotuba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Kwanza kabisa niseme kwamba Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi tunamfurahia kwa approach yake ya kwanza aliyoifanya alipokutanisha wafugaji wa Wilaya ya Same na Jimbo la Mlalo na wa kutoka sehemu zingine za Mkoa wa Tanga, akakaa na wafugaji, akaongea nao vizuri takribani wiki tatu, nne zilizopita. Amevunja rekodi na wafugaji wale walifurahi sana kwa mara ya kwanza kuweza kukutana na Waziri na kueleza matatizo yao na Waziri akawasikiliza na akaahidi kufuatilia na kuwapa ushirikiano mkubwa. Sioni kama kuna ubaya wa kumsifu mtu ambaye amefanya kitu kizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi nataka tu niseme machache maana mengi yamesemwa katika Kambi ya Upinzani ambayo yalikuwa katika yale niliyotaka niyaulizie. Kwa uchache huo ninalotaka kuuliza ni kwamba naomba Waziri ajaribu kunieleza kwa vile Serikali yetu inaangalia kukuza viwanda na ninaamini kwamba sustainability ya viwanda inatokana na malighafi ya ndani ya nchi. Je, kumekuwa na mawasiliano na Wizara ya Viwanda kuona jinsi ambavyo viwanda vile vitakavyotumia malighafi, yale maeneo yatakayotoa malighafi wale wakulima wanasaidiwa ili kuwe na mikataba maalum ya kuonyesha kwamba watatoa mazao yatakayoweza kufaa katika viwanda vile ili viwanda vyetu viweze kuboreshwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nauliza hivyo kwa mfano, nikianza na viwanda vya ngozi, kwanza tunaona kiwanda kile cha Kawe kilikufa hatujui kama kuna mpango wa kukifufua ama vipi lakini wafugaji wameshaandaliwa ili waweze kufuga ng‟ombe wazuri watakaotoa ngozi nzuri itakayotumika katika viwanda vyetu? Maana kama hakuna uwiano au mahusiano ya kupanga mikakati kati ya Wizara hii na Wizara ya Viwanda sioni jinsi ambavyo viwanda vyetu vitafanikiwa kama Wizara ya Kilimo na Mifugo haikufanikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kadhalika upande wa mazao yale kama pamba, kama tunataka kuanzisha viwanda vya nguo, je, wakulima wa pamba wameangaliwa jinsi ya kusaidiwa kwanza kulima, kuhifadhi na kusafirisha mazao yale kwenda kwenye viwanda? Tumeshuhudia viwanda vya Mwatex, Kilitex, Urafiki vyote vikifa au vikisuasua na sasa tunataka kuanzisha viwanda ambavyo sijui kama vinaangalia hayo yote. Maana wenzangu wachumi watanisahihisha kwamba lazima tuwe na backward na forward linkages otherwise kila Wizara ikifanya kitu chake parallel hakika lengo hili halitafikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, for example nimeona Kambi Rasmi wakitoa maelezo kwamba ukame umeathiri upatikanaji wa mazao kipindi kilichopita. Je, Wizara ya Maji inahusishwa katika sehemu ile itakayowekwa viwanda ili maji yapelekwe kwenye zile malighafi tusitegemee kilimo cha mvua? Wenzetu wa Israel wanatumia sana teknolojia ya drip ambayo inatumia maji kidogo sana lakini inahakikisha mazao yao yanakuwa bora sana. Je, Wizara ya Kilimo ina mpango wa kuongea na Wizara ya Maji ili wawekewe maji kule ambako wanataka kuboresha mazao yale ili system ya drip angalau ifanyiwe utafiti na sample kama kutengeneza model ya shamba ambalo linatumia drip na kuona wale ambao hawatumii system hii na wale wanaotumia nani ambao wanapata mazao zaidi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana kabisa kwamba Wizara hii ni nyeti na kubwa sana ambapo Watanzania wengi wanaitegemea. Tunaamini kwamba hata wale wanaojiita mabaunsa bila chakula hawawezi kuwa mabaunsa, kwa maana hiyo njaa haina baunsa. Kwa hiyo, naamini kwamba Wizara hii itaongezewa fedha ili kusudi iweze kufanya vizuri na itatoa mchango mkubwa ambao utakuwa input katika Wizara zetu nyingine kama zile za Afya na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia kwamba muda si rafiki, napenda tu nijue kuhusu kiwanda cha tangawizi kule kwenye Jimbo letu la Same Mashariki ambacho kimekuwa hakianzi kufanya kazi pamoja na Rais wa Awamu iliyopita kwenda kukifungua mwaka 2012. Matokeo yake wakulima wengi wa tangawizi ambao waliongeza sana kilimo cha tangawizi wamepata hasara kubwa sana na kule sasa hivi tuna makaburi mengi ya tangawizi kuliko ya wananchi waliofariki kutokana na kwamba wakulima hawakuwa na jinsi bali kuzika zile tangawizi zao. Sasa tunapowaeleza wakulima waongeze kilimo wakati hatujui jinsi ambavyo viwanda vyetu vitawahudumia hatuoni ni kuwasumbua wakulima bure?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka nimuulize Mheshimiwa Waziri, ana habari kwamba Rais wa Kenya ameruhusu kilimo cha mirungi na kutenga dola za Kimarekani milioni mbili ili kilimo hiki kikuzwe. Tukizingatia kwamba tuko katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, je, pamoja na kwamba sisi tumezuia kilimo hiki tunahakikishaje mirungi hii haitaingia kwetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafikiri ni vizuri Waziri wa Kilimo akawasiliana na wenzake Kenya kuona kwa nini wao wameruhusu zao hili. Naamini kwa vile wamejua lina faida sana na ni rahisi kuzuia madhara kama ukiruhusu zao hili kuliko ukilikataza halafu watu walime kwa kificho, watalitumia vibaya zaidi. Tuna mfano wa nchi ya Holland waliidhinisha maduka fulani kuuza dawa hizi za kulevya kwa kuamini kwamba wale watumiaji watatumia kidogo kidogo kuliko wakificha halafu watumie kwa wingi kwa wakati mmoja madhara yake yanakuwa makubwa zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme hivi, namshukuru Waziri wetu kwa mikakati hii mizuri lakini pia azingatie maoni ya upinzani maana yatamsaidia kuboresha kilimo, ufugaji na uvuvi ambao ni tegemeo kubwa sana la nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka pia nijue, je, Waziri wetu wa Kilimo ana mahusiano gani kupitia labda Wizara ya Viwanda na hili Shirika letu la World Trade Organisation kuona kwamba na sisi masoko yetu yanafiki katika kiwango kizuri cha juu na tukapata upanuzi wa masoko nchi za nje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda nisisitizie upande wa uvuvi, hizi neti ambazo ni ndogo na zinaharibiwa kila wakati, kwa nini ziruhusiwe kuwa nchini kama zinaleta madhara makubwa? Nafikiri Wizara waangalie na kuona kwamba neti hizi zisiruhusiwe ili tusitie wavuvi wetu hasara ya kuwachomea neti walizozinunua kwa gharama kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA – MWENYEKITI KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nichukue nafasi hii kuwashukuru wachangiaji wote wa hoja hii tuliyoileta mbele yenu, Taarifa hii ya PAC, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote mliotoa maoni yenu mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, sijaambiwa napewa muda gani!
NAIBU SPIKA: Una nusu saa Mheshimiwa lakini ukitumia muda pungufu ya huo utakuwa umefanya vyema zaidi.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA – MWENYEKITI KAMATI YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Muda niliopewa nusu saa na wachangiaji walikuwa zaidi ya thelathini, nikienda kwa kila mmoja, nadhani hatutamaliza leo, kwa hiyo, nitayaweka kwa mafungu kutokana na jinsi wachangiaji walivyochanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza wachangiaji wote walitupongeza Kamati zetu zote mbili za PAC na LAAC, tunawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, wachangiaji wote niliowasikia wamekubali kwamba PAC bila kuwezeshwa hatutaweza kufanya kazi yetu kikamilifu. Kwanza kwa sababu tukifanya ripoti tu kama tunavyoletewa bila kuwa na muda wa kwenda kuhakiki tutakuwa hatuwatendei haki waliotutuma kazi hii.
Kwa hiyo, ni wazi kwamba PAC lazima tukiletewa taarifa tuweze pia kwenda kuhakiki. Kwa hiyo tunaomba kama Bunge lako likaridhia kama kweli PAC inahitaji kuongezewa pesa ili ziweze kufanya kazi yake kikamilifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, wachangiaji wengi walisema kwa msisitizo tena kwa masikitiko, kuhusu jicho letu Wabunge, CAG ambaye bajeti yake ni ndogo sana kiasi kwamba hawezi kwenda kutembelea ile miradi mbalimbali maana ukisema tu sisi tufanye kazi, PAC kazi zetu zinategemea CAG analeta nini. Kama CAG hawezi kwenda kufanya audit ina maana PAC hatuna kazi. Kwa hiyo tungeomba sana CAG bajeti yake iongezwe, vinginevyo tutajidanganya Wabunge hapa na kazi hazitakwenda. (Makofi)
Mifuko hii ya jamii imeongelewa sana kwa uchungu na wachangiaji, Waheshimiwa Wabunge mbalimbali na Waziri amejaribu kujibu. Hata hivyo, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri na kusema kwamba walikuwa wanahakiki wafanyakazi hewa na amesema PSPF wameshamaliza, swali langu ni kwamba kama wamemaliza kwa nini hawapeleki, hawarudishi yale madeni ya PSPF ili waendelee kulipa mafao ya wastaafu?
Wastaafu wengi wamelalamikia sana sehemu hii kwamba mafao yao hawalipwi. Wabunge wengi wanapigiwa simu, mimi mwenyewe napigiwa simu kutoka Jimboni kwangu. Kwa hiyo tungeomba, sana kama wamemaliza na wanaendelea na Mifuko mingine, basi angalau Mfuko huu wawape pesa zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, kuna sehemu nyingine ambazo zinahitaji msisitizo kidogo. Suala la Lugumi ni suala ambalo limetuletea matatizo sana kwenye Kamati, maswali yamekuwa mengi kabla hata haijaundwa Kamati Ndogo na bahati mbaya Kamati yetu hadidu ya rejea yetu ilikuwa inatufunga sana kwenda kuhakiki kama vile vyombo vilinunuliwa na kufungwa ndiyo tulitumwa hivyo.
Bahati mbaya hatukuwa na mkataba kwa hiyo hata kama tumekuta upungufu mengine hatuwezi kuyaingilia, lakini kibaya zaidi tulikuta vifaa vingi kweli vimelundikwa, havikufungwa sasa je, ni vya mradi huu au ni vya mradi mwingine ili tukipita vinaondolewa vinapelekwa kunakohusika? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama vilinunuliwa kwa nini havikufungwa? Kwa nini kazi haikuanza? Miaka yote hiyo tangu 2011 mpaka leo miezi mitatu vifungwe? ndiyo kazi kubwa tuliyokuwa nayo. Kamati yetu wameshindwa kujibu maswali mengine tunayokutana nayo, ni sawa na mtu amefungwa miguu na mikono halafu anaambiwa kimbia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba, maswali ambayo bado Kamati ilijiuliza baada ya kupata ile Taarifa ya Afisa Masuhuli 28/10; ni je, vifaa vilivyoharibika kabla havijatumika ilikuwa ni wajibu wa nani avitengeneze ndipo vifungwe? Iweje Serikali inasema inasubiri ipate hela za bajeti za mwaka 2016/2017 ndipo ivitengeneze. Hilo ni jibu ambalo hatujalipata bado. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine tulikuta vyumba ni vichafu sana, sehemu nyingi vilipowekwa hivi vyombo, je, lilikuwa ni jukumu la nani kutengeneza? Hatujui. Kwa hiyo Kamati yetu ilifanya kazi katika mazingira hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, samahani ninywe maji maana hili ni tatizo kubwa sana. Hili tatizo limeninyima usingizi, tunapigiwa simu kwamba ooh tumekatiwa chochote au tumetiwa mifukoni. Ninachotaka kusema Waheshimiwa Wabunge, kama kazi kubwa ya vifaa vile ilikuwa kuchukua picha za wahalifu pale kituoni, kuhifadhi taarifa, kwa nini hizo kazi kubwa mbili hazikufanyika miaka yote hiyo? Je, hivi vifaa vilikuwa vinafanya kazi kweli? Maana hii kazi ya kusema Mkongo wa Taifa ulikuwa haujafungwa ili kuwa na mawasiliano, hii ilikuwa stage ya mwisho, lakini ulitakiwa ukifika kituoni ukute picha, taarifa…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ili utusaidie sisi ambao si Wajumbe wa hiyo Kamati, haya maswali unayoyauliza saa hizi anayepaswa kujibu ni nani, kwa sababu maswali ya Wabunge wote hawa ni wewe Mwenyekiti ndiye unatoa ufafanuzi ndio waliyekuuliza. Sasa na wewe ukiuliza mimi sina majibu, mimi siyo mjumbe wa Kamati, kwa hiyo nataka kujua. Kwa sababu Serikali haitapewa tena nafasi tutaelekea kwenye mapendekezo mliyoleta kwenye hii ripoti yenu.
Kwa hiyo utusaidie vizuri ili baadaye Bunge hili litakapokuwa linafanya maamuzi kwenye yale mliyopendekeza humu liwe na taarifa za kutosha. Utusaidie tu hicho Mwenyekiti kwa sababu Bunge hili linawategemea ninyi. Sasa ukiuliza maswali na sisi hatuwezi tena kujijibu; inabidi utujibu wewe mwenyewe.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA – MWENYEKITI KAMATI YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na nilikuwa nihitimishe hivyo, kwamba ndiyo maana tumesema! Umeniwahi tu. Ndiyo maana tumesema hatuwezi kutoa majibu yoyote hapa kwa taarifa tuliyoletewa tarehe 28 mwezi Oktoba; wakati tunafunga taarifa yetu mpaka tutakapoweza kuhakiki kama kiti chako kilivyotuambia kwamba, tuhakiki hivi vifaa kama vimefungwa.
Kwa hiyo, ndiyo maana nilitaka kwamba hii ajenda haijafungwa, huu mjadala haujafungwa, tutakwenda kipindi kinachofuata kuhakiki, kwa hiyo tutaweza kuleta taarifa kamili; hivyo ndivyo ilikuwa nihitimishe.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka kulizungumzia ni suala la TIB. Labda niseme tu kwa ujumla kwamba majibu ya Mawaziri nimeyapata mengine yameniridhisha kiasi, maana kasema hizi hoja tutakutana nazo wakati CAG atakapopitia yatakuja. Hata hivyo, mahali ambapo bado pamenipa utata ni ukiangalia jibu ambalo alilitoa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, kwamba kuna sheria ambayo inakataza mabenki kutoa taarifa za wateja wao.
Nikajiuliza kama hivi ndivyo, hivi hii taarifa ya TIB tuliletewa kwenye Kamati ili iweje? Imeletwa kwa minajili gani? Kupewa taarifa watu wamepewa hela, watu hawalipi, leo nahoji tujue zile kampuni ambazo zimepewa hela hizi, miaka hawalipi tunaambiwa hapana, hamuwezi kufanya hivyo, hawawezi kutoa siri za wateja. Hizi pesa kwanza ni za nani? TIB inawajibika kwa nani?
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema Spika amefanya makosa kutojua hiki kifungu kwa vile ameshawaandikia TIB kwamba watuletee hizo taarifa za yale mashirika sugu yanayodaiwa ambao hawajataka kuleta hizo taarifa tukaziona ili Bunge lako likatoa maagizo kwamba wachukuliwe hatua gani. Je…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, umemtaja Spika, hapo kwamba pengine hakukijua hicho kifungu; kifungu anakijua, maagizo aliyotoa haimaanishi ninyi mtaletewa hiyo taarifa moja kwa moja ndio utaratibu ambao tunautumia siku zote. Kwa hiyo si kwamba kifungu hakikujulikana ama hakukiona, anakifahamu kifungu na ametumia sheria nyingine kuitisha ile taarifa. Itakapomfikia yeye ataangalia namna bora ya kuileta kwenu kama ni taarifa ambayo inapasa kutolewa basi atawaletea. Kama ni ile ambayo haipaswi kutolewa basi hatoileta; tuendelee.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA – MWENYEKITI KAMATI YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru lakini naomba uniache kwa vile Kamati… (Makofi)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, inaniwia ngumu kwa sababu kwa maelezo yako wewe ndio unatusaidia tufanye maamuzi na maamuzi lazima tufanye leo. Sasa nikisema nitapata muda wa kujibu baadaye sina na wewe ndio unayetusaidia ili tufanye maamuzi baadaye, Bunge zima hili linakutegemea wewe tu ndiyo mwenye hoja hii.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA – MWENYEKITI KAMATI YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Sitaki kubishana na kiti, lakini nimeshapata taarifa, lakini pia nilikaa nikajiuliza ambalo labda litaingia huko. Hivi wateja sugu wanapotolewa kwenye magazeti kwamba hawalipi maana yake nini? Nafikiri Waheshimiwa Wabunge, hiyo hoja tuiache, tusubiri Spika atakapotuletea ile barua na majibu yake tutajua tufanye nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, tukija kuhusu suala la na SACCOS. Mheshimiwa Mhagama amelijibu, nafikiri alikuwa anawajibu wale Waheshimiwa Wabunge waliosema kwamba NSSF isitoe mikopo kwa SACCOS; amelijibu vizuri. Kamati yetu tatizo lake lilikuwa si hilo, Kamati yetu tumesema tatizo hapa ni kwamba NSSF imeweka utaratibu wake kwamba, mkopaji au atakayekopeshwa atumie vigezo hivi. Kwanza imeweka ceiling kwamba kukopa ni kuanzia minimum ni milioni 50, maximum ni bilioni moja. Pia wakasema collateral lazima ionekane kwamba iwe ni 50% ya ile amount unayotaka kukopa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tatizo letu lilikuwa je, wale waliopewa zaidi ya bilioni moja mpaka bilioni mbili na laki tano, ni sawa sawa hiyo? Si sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kwa wale ambao wamepewa mikopo ambao hesabu zao zilikuwa hazijakaguliwa, lakini wakapewa mikopo, tukasema si sawasawa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, tukasema wale ambao hawajarejesha mikopo ile, maana pesa hizi ni za kulipa mafao ya wastaafu, hivyo si sahihi na ndiyo maana sisi tumesema, tunaomba CAG aende akahakiki akafanye ile kazi ili atuletee taarifa kamili. Nani wamelipa na nani hawajalipa, nani wamefanya kinyume ili iletwe katika Bunge lako au katika Kamati tuweze kuleta katika Bunge ili lichukuliwe hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, ya kuzungumza ni mengi nimerukia kwa Manaibu, ndiyo nilikuwa nakwenda nikiangalia hizi responses zilizotoka kwa wenzangu mbalimbali ambao wamechangia. Sasa naweza nikarudi nyuma kidogo kuzungumzia mengine ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyasema; ili kwamba hata muda ukiisha tutakuwa angalau zile important areas tumezipitia.
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wengine wamezungumzia kuhusu tatizo la bandarini kuhusu zile meli, kweli wamesema kama sisi tulivyosema kwamba inakuwaje meli iingie mpaka itoke miezi 18 taarifa zake hazijajulikana, hawajalipa. Hilo limezungumzwa na sisi tuliliweka katika taarifa yetu. Kwa hiyo tumesema kwamba bandari yetu inatakiwa iangaliwe kwa ukaribu sana ili iweze kufanya kazi zake kama inavyotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la TRA na misamaha ile ya kodi, pia tumeleta katika Bunge lako ili ijulikane kwamba TRA wapewe maagizo ili wafanye kazi zao. Kuhusu ile misamaha hewa watuambie wale ambao wana misamaha hewa wamechukuliwa hatua gani? Ndiyo maana tumeleta hilo ili nalo kama Kamati yetu ilivyopendekeza tupewe majibu kwamba wamechukuliwa hatua gani kwenye misamaha ile ambayo hawakukidhi, wengine ni misamaha hewa, ifanyiwe kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mengine kwa kweli in general yamezungumzwa sana hayo ya kuhusu TR na kuelezea jinsi ambavyo Kamati yetu imependekeza kwamba TR awezeshwe ili na yeye aweze kufanya kazi yake vizuri. Tunampongeza sana kwa kweli ameisaidia sana Kamati yetu na hivyo tunaamini kwamba atakavyozidi kupewa nguvu ataweza kuendelea kufanya kazi nzuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu haya Mashirika yetu ya EWURA, SUMATRA kwa kweli tumesisitiza na Waheshimiwa Wabunge wameliongelea kwamba zile tozo wanazoleta kule Serikalini hazikubaliki, kwamba wapunguze administrative expenses zao ili waweze kutoa tozo linalokubalika Serikalini.
Mheshimiwa Naibu Spika, mengine samahani kidogo mnisamehe, maana yameingiliana na ya wenzetu, ya LAAC lakini at the end of the day tunakubali kwamba, pesa za maendeleo kwa kweli Mheshimiwa Waziri wa Fedha ni vizuri ziende kama zinavyopitishwa na Bunge, otherwise nchi yetu tutapiga kelele hapa, lakini hatutapiga hatua, zipelekwe kwa wakati. Ili zile bajeti zinazopitishwa hapa zihakikishwe kwamba zinafika kule zinakotakiwa ziende.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Kilimo amejitahidi sana kuelezea aliyoyaelezea na kuhusu ile ya wafanyakazi kwamba wanaangalia sababu nyingine na kwamba hawakusimamishwa tu kutokana na yale mahindi mabovu, kwa hiyo, tunajua kwamba tutapata taarifa kamili katika ukaguzi ujao ili tuweze kujua hatma yao imekuwa ni nini. Hayo maghala aliyoahidi naamini yatajengwa ili yafanye kazi vizuri na nguvu ya wakulima isipotee bure.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri nimejitahidi ku-cover maeneo mbalimbali na naamini kwamba eneo kubwa la hii taarifa yetu masuala yake yalikuwa yamewekwa katika mafungu hayo niliyoyataja ndiyo maana nimeya-sum up.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kwamba Bunge lako Tukufu sasa lipokee na kukubali taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali pamoja na mapendekezo yaliyomo katika taarifa hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. Ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii tena ya kuweza kufanya majumuisho ya taarifa ya PAC tuliyoileta asubuhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kukushukuru tena wewe binafsi kwa kuongoza mjadala huu tangu asubuhi mpaka sasa hivi. Naomba pia niwashukuru wachangiaji wote waliochangia hoja hii; kwa kuwa wengi wanaunga mkono taarifa ya Kamati katika kusimamia matumizi ya fedha za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahili kwamba Waheshimiwa Wabunge wanachukizwa na matumizi mabaya ya fedha za umma. Wachangiaji waliochangia ni wengi akiwemo Mheshimiwa Allan Kiula ambaye amezungumzia mradi wa Mlimani City, Suma JKT, Polisi na TANESCO. Mheshimiwa Munde pia ameongea kwa undani mambo ya TANESCO na NSSF, Mradi wa Dege pamoja na Mlimani City, Mheshimiwa Catherine amezungumzia Mlimani city na NSSF. Wote hawa pamoja na wachangiaji wenzangu wengine ambao si rahisi kila mmoja kusema eneo lake.

Lakini Mheshimiwa Gekul amezungumzia mambo ya Pride, Mheshimiwa Mussa Mbarouk amezungumzia mambo yote yaliyoko kwenye taarifa yetu, Mheshimiwa Kigua mambo ya ALAT na Mheshimiwa Mabula umesisitiza ripoti ya Kamati Ndogo ambayo mwisho iliridhiwa na Kamati yote kwa Spika na pia akazungumzia mambo ya Mlimani City.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wenzetu wengine wamechangia kwa kuleta kwa maandishi ambao ni wengi na nafikiri majina yao ninayo. Walioleta ni pamoja na Mheshimiwa Rhoda Kunchela, Mheshimiwa Mary Muro ameleta pia, Mheshimiwa Ritta Kabati, Mheshimiwa Lucia Mlowe na wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipende kutoa masikitiko yangu kwamba Kamati, especially hii yetu ya PAC na LAAC tunapewa muda mfupi sana wa kushughulikia hesabu hizi za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma pamoja na Serikali za Mitaa. Kwa uzoefu wenzetu wa Mabunge mengine hata ukienda Bunge la Uingereza unakuta kazi ya PAC ni ya kudumu, wana ofisi wanayofanyia kazi kwa muda kwa hiyo wanajipanga vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi muda tunaopewa ni mdogo sana. Wiki mbili uwe field, wiki moja uandae taarifa ulete hapa. Kwa hiyo, unakuta tija ni ndogo mno. Hatuwezi kuitendea haki kazi inayofanywa na CAG ya mashirika zaidi ya 200 halafu tukakaa hapa kwa nusu siku tunaongea taarifa za CAG za mashirika yote hayo pamoja na Serikali Kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na ripoti zote na ripoti yoyote ambayo tumeileta na reaction za Waheshimiwa Wabunge na Mawaziri, niseme kwa kiwango kikubwa ripoti yetu imekubaliwa. Niwashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina machache tu ya kuongea. Mheshimiwa Waziri wa Fedha ame-cover mambo ya Benki ya Azania, Pride na amesema yanashughulikiwa. Nina maeneo mawili ambayo nataka kweli tuyazungumze kwa kina kuhusu hoja ya Mlimani City ambayo pia Waziri wa Elimu amejaribu kuyaeleza na kuelezea jinsi ambayo Chuo Kikuu kinafaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kusema kwamba tunakubali vitu vidogo vidogo sana. Ukipewa shilingi bilioni mbili mwenzio akichukua bilioni 20 unaona ni sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nasema tumedhulumiwa sana katika project hii ya Mlimani City. Hoteli ya nyota tatu yenye vyumba 100 ilitakiwa iwe imeisha tangu mwaka 2006. Hebu hesabu ni pesa ngapi tumepoteza tangu hapo mpaka leo,?

Mheshimiwa Mwenyekiti, botanical garden ilitakiwa iishe mwaka 2006. Pesa kiasi gani tumepoteza ambazo kulikuwa kuwe na tourism pia mpaka leo bado tunasifu kwamba mwekezaji anatupa chochote, sisi tumekuwa watu wa chochote, inasikitisha sana. (Makofi)

Nipende kusema tuwe na uchungu wa nchi yetu. Huyu mwekezaji amesema kwamba wanamshinikiza aje akae waongee, hebu ona anashinikizwa! Mtu aliyekuja na dola 75 leo anashinikizwa ili aje aongee matatizo haya. Kama kweli ameweka pesa nyingi katika mradi huu kwa nini ashinikizwe? Tuna mambo mengi ya kujiuliza juu ya Mlimani City. Inawezekana hata huyo mwekezaji hayupo, ni watu wachache wamejichukulia jina akasema ni mzaliwa wa Botswana anaishi South Africa, lakini hata kwenye Kamati juzi hakuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtu ameweka pesa yake nyingi hivi, structure zile asionekane kwa nini? Na bado tuichukulie juu juu. Mimi nasema kwa hili bado Kamati ilivyoshauri kwamba ufanyike ukaguzi wa kiuchunguzi, nasema Bunge lako liridhie ifanyike forensic and performance audit. Nasikitika na naona uchungu, naomba maji maana nasikitika jinsi ninavyoona Serikali inachukulia jambo hili kijuu juu, tunajaribu kuli-water down. Ardhi yote ile imechukuliwa, mikataba inaongezwa kidogo kidogo. Mkataba haujaisha umeongezwa, umesahihishwa na bado tunaongea, tunafurahi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri hata mtukufu Rais akisikia hili atasikitika sana na atasikitika jinsi ambavyo Watanzania tunatetea wawekezaji. Kamati tumejipinda bila overtime bila nini, tunafanya kazi. Hata tuliposema hatuna muda wa kutosha wa kufanyia kazi tukawaambia hapana leteni hivyo hivyo hiyo ripoti yenu. Bado tunakuja hapa Serikali inatetea kwamba mwekezaji anafanya vizuri katupa shilingi bilioni mbili, inatosha. Yeye akichukua hata shilingi bilioni 40, sisi tukipata shilingi bilioi mbili inatosha! Kweli katika awamu hii tunataka kwenda kwenye viwanja, tunataka kukusanya hela, tunaweza kutetea hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu angalia, nafikiri Waziri wa Viwanda na Biashara ataeleza jinsi ambavyo CBE imetoka mahali ambapo ilikuwa inapata ruzuku kutoka Serikalini sasa hivi inajitegemea na uangalie university mpaka sasa hivi inasaidiwa kujenga hostel, lakini tuna mradi ambao ungeweza ukajenga hostel hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu angalia wanafunzi wetu wanapelekwa Mabibo, wana-cross barabara wanaibiwa computer, wangetakiwa wafanye kazi mpaka usiku wakiwa kwenye lecture rooms’ lakini wanashindwa wanaondoka mapema maana hapo Ubungo kupita mpaka Mabibo wanaibiwa. Hostel inajengwa nje ya chuo wakati nafasi kubwa ilikuwa pale, eneo kule lile. Lile eneo ungetegemea ndiyo zijengwe hizi hostel tukaona tuwekeze, leo tunakuja na neno la kwamba tunapata bilioni mbili.

Waheshimiwa Wabunge, naomba nielezee hivi; hii hela tunayoambiwa Chuo Kikuu wanapata bilioni mbili, naombeni mnisikilize. Chuo Kikuu wameshindwa kufunga mahesabu yao tangu 2014. Kamati imehangaika nao, ilikuwa ifikie hatua mbaya sana, lakini sisemi mengi.

Mwaka 2014 hawajafunga hesabu, 2015/2016 hawajafunga hesabu na ni Chuo Kikuu Kikuu kinachofundisha wahasibu, Chuo Kikuu cha nchi chenye hadhi hiyo. Sasa hata hii hela tunaambiwa inaingia huko kutoka Mlimani City, tuna uhakika nayo gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba, tuna muda mfupi wa kuzungumzia mambo haya lakini forensic audit inavumbua mambo mengi sana. Tutataka wote waliosaini huu mkataba waonekane, wazungumze, huu mkataba waliousaini hivi ulikuwa na maana gani? Halafu ukisoma ule mkataba ulikuwa haufungamanishi ujenzi wa Mlimani City na barabara ya Sam Nujoma. TIC wanawaongezea kwamba barabara kweli ilichelewa, wakati ujenzi haukuwa na mahusiano yoyote na barabara ya Sam Nujoma. Kwa hiyo TIC nao wanaingia hapo, Serikali, inaingia kati inamuongezea huyu mwekezaji muda kila leo. Mkataba haujaisha, umeongezwa mwingine, hivi tuieleweje nchi hii? Kwa hiyo TIC wanahusika pia katika kuhujumu nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikataba imeongezwa kiaina aina, tena correspondences tunazoziona ni kwa e- mails; hebu fikiria mtu mwenye hela yake nyingi hivi, hapo South Africa anafanya kwa e-mail. Juzi tulimuita kwenye Kamati tunataka tumuone mwekezaji, hakuonekana! Katuma Meneja wake, tukimuuliza swali anasema ngoja nikapige simu nimuulize mwekezaji. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili tunadharauliwa vya kutosha. Hii Kamati imeundwa na ninyi, ni sehemu ya Bunge, auditor anafanya kazi kubwa, anaeleza matatizo halafu tuliokosa uzalendo tunakuja hapa tuna water down, hivi unatetea nini? Hivi kweli Rais Magufuli akiona hili atafurahi kweli kwamba tunatetea kitu hapa. Kwa kweli nasema personal interest tuziache. (Makofi)

Mimi nasema, hilo naomba, kuna mambo mengi sana Waheshimiwa Wabunge ambayo hatuna muda wa kuyaelezea kwenye hizi documents zote. Muda tunaopewa, napewa nusu saa kuelezea mambo yote yaliyofanyiwa audit, kwa nusu saa tu! Kweli naweza kufanya justice katika Idara hii? Hapo hapo mjue hatuna ofisi, kila mmoja anakaa na documents zake nyumbani, ukitafuta hili unachambua siku nzima, hujapata unalitafuta! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba kusema kwamba naomba tuombe ufanyike uchunguzi wa kitaalam tangu uanzishwe mradi huu waliosaini akina Profesa Luhanga, nafikiri wako hai na TIC ilivyoingia hapo ndani mpaka hapa tulipofika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI ameeleza mambo kwa ufasaha najua ALAT unaifanyia kazi kwa hiyo tutangojea matokeo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuingie kwa Waziri wa Mambo ya Ndani. Waziri wa Mambo ya Ndani amekuja hapa ameeleza mambo ya magari haya na mikataba ya NIDA, mikataba ya immigration. Nikiongelea hili la magari tumehangaika nalo tangu mwaka wa jana tukiomba mikataba tunapigwa danadana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati tunaomba mkataba ambao unaruhusu pesa zitumike ambazo hata kama ni deni nchi italipa! Tunapigwa dana dana. Kwa hiyo tunafanya kazi bila vitendea kazi vilivyokamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais kwa kwenda hapo bandarini hailizuii Bunge kuunda kamati ya uchunguzi ikafanye kazi yake. Ijulikane wazi kwamba kama Mheshimiwa Rais asingekwenda juzi ina maana wenzetu Wizara wangekuwa bado wanalifumbia macho. Hili tatizo hatukulileta jana au juzi, lililetwa tangu mwaka jana. Tumempa Afisa Masuuli nafasi mara tatu, akija anatupiga danadana mara apite huku, apite huku. Vile vitu tunavyomwambia, atuletee, documents hizi na hizi, hataki kuleta! Sasa hayo mambo yalikuwa wazi kwanini hakuleta ile mikataba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi hatuzungumzii kwamba risasi ngapi ama bunduki ngapi ziliingizwa, tunazungumzia fedha za umma inakuwaje iwe ngumu kuleta taarifa kamili ili tulione hilo na kuangalia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Waziri anaposema eti, wameunda Kamati zinachunguza, hivi kweli mtu anaweza kujichunguza mwenyewe? Kwani hayo magari yameletwa mwaka huu? Kwanini huo uchunguzi angoje mpaka Mheshimiwa Rais aende ndipo aunde uchunguzi? Kwa hiyo ni wazi kwamba Wizara ilikuwa imelifumbia macho na wanajua kilichokuwa kinatendeka. Sasa haya yote yanayozungumziwa hapa mimi nasema Bunge lako Tukufu liazimie kwamba ukaguzi wa kiuchunguzi ufanyike. Hatuwazuii wao kufanya kazi yao wanayotaka, wakitaka kufanya kazi yao waendelee, lakini Bunge lijiridhishe kama makinikia ilivyofanyika na hii ifanyike hivyo hivyo, ieleweke kwamba kuna nini hapa. Kwa vile kuna mambo mengi inaelekeza yamejificha, sasa sisi tutafanya cosmetic, lakini tunataka tuingie ndani ya mzizi huu wa tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipokuwa tunataka kuongea mambo ya NIDA tukaambiwa kwamba kesi iko Mahakamani. Kwa hiyo, hata mkataba hamuwezi kuletewa, zaidi ya hapo tukaambiwa hii iliyowekwa sasa hivi ni addendum, hamuwezi kuongelea addendum kama hamkuingia kwenye mkataba wenyewe. Sasa ni kama PAC tumefungwa miguu na mikono. Kila ukitaka kuangalia hiki unaambiwa hapana. Mambo ya Ndani ukitaka kuangalia hiki unaambiwa hapana. Lakini mbona Jeshi la Wananchi wa Tanzania tukiwaambia leteni hiki wanaleta? Jeshi wanaleta, haya ya Mambo ya Ndani kwa nini yanakuwa mazito? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunaomba Bunge lako Tukufu liridhie kwamba kuna mambo ambayo yamefichika ambayo kama tukiyachukua juu juu kwa maneno ya kisiasa tutakuwa hatumsaidii Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli. Tunataka uchunguzi ili Mheshimiwa Rais yawe mezani kwake! Bunge likishajua ajue kuna nini mbivu na mbichi zijulikane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya passport, immigration; Kamati imezungumzia kwa undani jinsi pesa za visa zinavyopotea, kwamba mtu akikata visa Marekani au Ufaransa au Dubai au wapi haijulikani na upotevu wa pesa nyingi uko katika visa. Sasa leo tukiongelea tu passport, hata zikarembwa kiasi gani, zikawa nzuri kiasi gani wakati hakuna jinsi ya kujua kwamba pesa ya visa imeingia kiasi gani, tunafanya kazi gani?

Mmh, mambo mazito haya lazima ninywe maji.

Kwa hiyo tunaomba kwamba tuyaangalie haya mambo kwa undani. Nia ya kwenda kwenye uchumi wa viwanda inataka tuwe na hela. Kama tunataka kuwa na hela lazima tuangalie kule kote ambako pesa yetu inapotea. Sasa kama hatuingii kuangalia visa zinalipwaje, je, wale wanaoingilia airport pale wanalipa kiasi gani, zinawekwa wapi na zinawekwaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna data ya kuonesha kwamba kuna kusomeka mtu akichukua visa akiwa South Africa au akiwa Uarabuni wakikaa ofisini pale wanaona watu wangapi leo wameingia Tanzania na wamelipa kiasi gani. kwa hiyo tusiremberembe mambo hapa kwamba passport nzuri sana, hata gauni yangu hii nzuri. (Makofi/kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama hatuzungumzii mambo ya msingi tukizungumzia vitu vidogo vidogo kwamba hiki kizuri, hii hata kama ingekuwa nzuri kiasi gani mbona hata Marekani wanaweza kukakatalia usiingie kule kwenye nchi yao, hata kama ingekuwa nzuri kiasi gani. (Makofi)

Kwa hiyo tuangalie mambo kwa undani, tunafanya kwa awamu, awamu ingeanzia basi kwenye immigration ili tujue pesa imeingia kiasi gani. Ili tujue basi tutengeneze passport nzuri maana tuna hela, tunaanza vice versa kwa nini? Ninaomba tuangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongea kwa juu juu sana mambo mengi maana tukisema tuingie ndani kwa muda ulionipa nitakuwa siwezi kumaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie tu utata ambao ulitokea kati ya Wajumbe wangu wa Kamati ambayo mmoja anasema heka moja ilinunuliwa milioni 800 mwingine anasema sio hivyo. Ni kwamba wanaweza hawa watu wakawa wanaongea kitu kimoja isipokuwa mmoja anaongea land for equity mwingine anaongelea cash money. Hili jambo ukitaka kulieleza sasa hivi sitaweza kulizungumzia maana la kihasibu zaidi, lakini itoshe kusema kwamba…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kaboyoka tafadhali kidogo naongeza dakika 30 kwa mujibu wa Kanuni ya 28(5) endelea.

MHE. NEGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE HESABU ZA SERIKALI:
Mheshimiwa Mwenyekiti,ahsante sana. Hapo awali huu mradi wa mradi wa dege ulikuwa mwekezaji alisema ana hekari 20,000 ambazo ndio alikuwa ameweka katika mradi. Baada ya auditor kufanya kazi akaonekana ana heka 300 tu. Kwa hiyo si hekari 20,000 ana heka 300; kwa hiyo pungufu ya hekari 19,700. Sasa hawa watu wawili ni wahasibu, mmoja kachukua hesabu za mwekezaji alisema nini mmoja akachukua land for equity kwamba ile land ilipewa thamani ya kiasi gani, lakini wote walikuwa wanaongelea jambo moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda tu itoshe tu kusema mradi huu umekuwa na utata, mradi huu ripoti yake Kamati Ndogo walienda kuungalia kwa undani, ukaletwa ripoti kwenye Kamati nzima ya PAC tukaupitia. Uliangaliwa kwa kina na ukatengenezwa mapendekezo yake na kama alivyosema Mheshimiwa Mhagama ripoti ikapelekwa kwa Mheshimiwa Spika. Ripoti ilipelekwa tangu Februari, 2017. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme kwamba hii ripoti imezungumzia mambo mengi ambayo siwezi kuyasema kwa muda huu mfupi na ndio maana Kamati ikasema, Mheshimiwa Spika ailete ile ripoti iangaliwe ili Bunge liweze kutoa maazimio. Kwa mantiki hiyo na tunajua kwamba Mheshimiwa Spika hayuko nchini, kwa hiyo tukashindwa kwamba turudie tena mapendekezo yale yale na ina maana tunge-rewrite ile ile ambayo tayari iko kule kwake tukaona kwamba Kamati tutakuwa tunajichanganya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nawaombeni Waheshimiwa Wabunge tuvute subira, Mheshimiwa Spika atarudi, hii ripoti itaangaliwa kwamba inasemaje. Kwa hiyo, tumeshindwa sasa hivi tusemeje isipokuwa tumesisitiza tu kwamba yale mapendekezo kamati iliyotoa kwenye ripoti ile yafanyiwe kazi na hapo yatakapoletwa Waheshimiwa Wabunge tutaweza wote kuiangalia na ku-debate.

Kwa hiyo niseme kwa kifupi kwamba kwa muda ulionipa niliogopa nisichanganyikiwe kama asubuhi ambayo nilikuwa na mengi ya kuongea na sikuweza kuhitimisha sasa nitajipeleka kwenye kidogo ili niweze kuzungumza yale machache ambayo ningeweza kuzungumza pamoja na kwamba kuna mengi ambayo ningeweza kuzungumza lakini itoshe na naona umeshanipigia kengele nikushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Wabunge wengine waliochangia ambao kwa kweli haikuwa rahisi kuwataja wote kwa sababu ya muda nashukuru kwamba mmenisikiliza Waheshimiwa Wabunge hivyo basi Kamati inashauri Bunge lako kukubaliana na mapendekezo ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kauwa maazimio ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnataka nirudie au?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hivyo basi Kamati inalishauri Bunge lako Tukufu kukubaliana na mapendekezo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuwa Maazimio ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, suala la pango limeongelewa sana labda sitalirudia rudia sana, lakini niseme tu kwamba hata ripoti ya CAG tangu nimekuwa Mwenyekiti wa Kamati hii mwaka wa sita sasa imezungumzia sana fedha nyingi inayopotea kwenye kulipia fedha za pango kwenye Balozi zetu mbalimbali. Ni wazi kwamba fedha zile zingekuwa tumejenga ofisi zetu, kwanza mpaka sasa hivi tungekuwe tumeshamaliza na ofisi zile zingepangishwa.

Mheshimiwa Spika, lakini niseme pia kwamba pamoja na hayo, ukiangalia kwa mfano Ubalozi wetu wa Washington, Mheshimiwa Liberata Mulamula - Waziri wewe nakufahamu sana na cv yako ni nzito hebu tembelea Ubalozi wetu tena uangalie. Inasikitisha na ni aibu, yaani jengo limechakaa, ni aibu furniture ni za zamani, labda ziwe zimewekwa mwaka jana ambapo sijakwenda. Lakini hata ukifika pale layout yake inatisha, yaani unatoka Ubalozi wa Kenya, uone wenzetu walivyopanga ofisi zao za kibalozi, ingia yetu ya Tanzania, utafikiri tupo ofisi ya Kariakoo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nakuomba sana tukaangalie hizi balozi zetu jinsi ambavyo zipo katika hali mbaya na ya aibu. Hiyo itatuwezesha kuona umuhimu wa kujenga majengo ya kisasa ambayo ni mazuri na kuweka furniture ambayo inayoendana na nchi yetu ambayo tumesema tunaingia katika uchumi wa kati.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo maadili ya staff, nimekwenda kwenye balozi nyingi nyingi kitu ambacho nime-observe bado sisi sio staff wote, lakini pale unapokutana nao kwenye mambo ya visa kuna rafiki zangu wanasema hebu tukusindikize kwenye ubalozi wenu tukapate visa, utapata aibu. Sitawataja hapa maana si vizuri, lakini unakuta watu wameweka maandazi, wameweka vitumbua, wamekaa wanakula, ukifika wanakuchekea, karibuni karibuni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtu amekuja yupo serious katoka labda state ya mbali, anataka ahudumiwe haraka haraka, lakini anakutana na watu wanacheka cheka, wameweka maandazi yao hapo, wanakula, hawana hata aibu. Sasa unasema hivi kweli ile shule yetu ya Diplomasia si inafundisha watu ethics, enheee kwamba mnajiwekaje, mkiwa kwenye ubalozi mna-behave vipi, lakini hilo kwa Watanzania sisemi ni wote, wala sisemi ni Balozi zote, lakini sijui kama Europe na Marekani kuna Balozi za wenzetu ambazo sijaingia. Kwa hiyo tuna tatizo hilo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nizungumzie watanzania wengine tunaokwenda kwenye delegation za nje. Hili halipo kwenye ripoti sijaliangalia, lakini zamani tulikuwa delegation ikitakiwa kwenda nje, Chuo chetu cha Diplomasia wanakaa nao wanawaeleza, sasa hivi ni wengi, lakini tuwe na mikakati ya kueleza watu wetu. Unakuta mmekwenda na delegation kikazi karibu three quoters wamekwenda shopping, mmekaa watu wawili/watatu pale. Tunaaibisha kwamba kweli tumekwenda kufanya shopping hatukwenda kwa ajili ya yale yaliyotupeleka kama mikutano, ni aibu kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia table manners ni kitu muhimu sana, ni kitu hatukiongelei lakini nataka tukiongelee. Unakuta mmepangiwa buffet, mtu anajaza lisahani mpaka chakula kinamwagika, enhee! Yaani wakati tungefundishwa huku kwetu tumezoea kujaza maana utakula mara moja basi, lakini kule wenzetu buffet urudi hata mara tatu/mara nne. (Makofi/Kicheko)

Nimgeomba sana tuwe na njia ya kutengeneza semina ambazo zinahamasisha au zinaeleza ethics za kwenda kula kule nje. Niliona moja niliaibika sana, mtu kaenda kachukua supu na mkate kaweka, kaenda kajaza chakula, alivyomaliza alisema sasa nishushie na supu sasa, yaani ile supu ya starter yeye ndio kafanya ndio ya kushushia. Sasa wanatuangalia kwamba hawa watu gani hawa, wametoka wapi! (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa hao ni Wanyamwezi, Wasukuma. (Makofi/Kicheko)

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, unaogopa kusema tumetoka Tanzania.

Kwa hiyo naomba sana yaani tuangalie hivi vitu vya kidiplomasia, it matters a lot kwamba tuna-portray picha gani tunapokenda nchi za nje.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tuangalie hii Sera ya Diplomasia ya Uchumi. Nimefurahi mlivyoonesha kwamba mnaifanyia kazi na mnaikamilisha. Mimi ningeomba tu, kwenye sera ile sijaisoma, kwa hiyo, siijui. Lakini nadhani tuwe na priority ya kuonesha kwamba mabalozi wetu tuna-identify, kwa mfano, Balozi aliyepo Uchina au Japan au New York au wapi tunakupa kwamba ututafutie wawekezaji kwenye maeneo hayo, tuwe specific ili mtu asiamue tu yeye huyu anakuja kutengeneza tu wine hapa na nini, kumbe tuna vitu vingi ambavyo vinge-create employment, viwanda kama vya pamba, tuchakate pamba, tutengeneze nguo, tu-add value kwenye products zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, which means Wizara ya Mambo ya Nje wakikaa na Wizara ya Viwanda na Kilimo wanaweza ku-prioritize zile areas ili wawape mabalozi kwamba hizi ndio areas ambazo tunaona mzipe kipaumbele wafanya mikakati ya ziada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzetu utakuta Wachina walikuwa nyuma sana, ni miaka kumi tu walitutangulia, lakini sasa hivi wanasaidia karibu Afrika nzima. Kwa nini, wao walilenga mwekezaji anayekuja wanampa conditions sisi tunataka uwekeze hapa, kama huwekezi hapa basi kwaheri. Halafu sasa sisi wewe unampa mtu, anaweka kakitu kadogo amechukua ardhi kubwa halafu returns zake hatuzioni.

Mheshimiwa Spika, area nyingine nakata kuzungumzia, sasa hivi tunataka ku-promote Kiswahili kuwa lugha ya Taifa na nchi nyingi za nje zimekubali zitumie lugha ya Kiswahili, lakini nakumbuka kuna chuo kimoja tu nafikiri ni Michigan, Mnigeria ndio anafundisha Kiswahili kule, wakati nafikiri tungekuwa na mipango mikakati kwamba ni sehemu zipi au vyuo vipi vinahitaji vya huko nje kufundishwa Kiswahili, tukaomba jinsi nchi yetu inavyoweza kutupia wale walimu wakapelekwa kule. Lakini hapo hapo na sisi kwa vile tunakwenda kwenye Kiswahili, unakuta lugha ya kingereza itatutupa nje. Sasa hivi lugha ya Kiingereza bado ni tata, je, tutakapoingia moja kwa moja Kiswahili itakuwaje.

Mheshimiwa Spika, zamani kulikuwa na wale volunteers from nchi kama za Marekeni, Uingereza na nakumbuka…

(Hapa kengele ililia)

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Nafikiri kengele ya kwanza hiyo.

Nakumbuka Waingereza walikuwa na retired officers ambao ni walimu na walikuwa tayari wapelekwe nchi za nje kama Tanzania waje wasaidie kufundisha Kiingereza ambacho mahitaji yao wao walitakiwa nyumba tu wala sio malipo. Hebu tuwape mabalozi wetu kazi za kuweza ku-identify hizi areas kuona kwamba je, hatuwezi kupata walimu wa kutufundisha Kiingereza propery. Maana ukiangalia sasa hivi hata mtu akitoa speech hakuna wale wenzetu makabila watanisamehe ambao “r” anasema “lailway” hasa nitasema “lailway” ni kitu gani ni “railway” hiyo. Sasa unakuta mtoto wa kwanza anafundishwa kingereza na mtu ambaye kwao hakuna “r” au Kiingereza chenyewe huyo anayekifundisha naye ni mbabaishaji, watoto wetu watajifunza lugha gani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo unakuta kwamba tunakuwa tuna-specialization kwamba sasa Kiingereza iwe tuna-specialize kwa hiyo tunakijengea mikakati au Kifaransa au Kichina tupate walimu wazuri wa kufundisha vizuri ambao watafundisha ile lugha kikamilifu.

Mheshimiwa Spika, sisi nchi yetu bado tuna nafasi sana ya ku-liaise na mabalozi wetu tukapata volunteers kama hatutaweza kuajiri walimu hao ambao wakatusaidia na pia hata kupeleka walimu wetu nje wapate exposure. Unakuta mwalimu anafundisha Kiingereza hajawahi kumsikia muingereza mwenyewe akiongea, kwa hiyo unakuta hata anavyofundisha inakuwa ni aibu.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mambo ya Nje ni kioo chetu kwa nchi za nje, kwa hiyo ningeiomba Wizara mtusaidie sana kuonesha kwamba Tanzania ni nchi yenye utajiri mkubwa sana, lakini tumekwenda zaidi katika ombaomba, tuna-feel proud tukiona nchi fulani inatusaidia, inatukopesha. Tutoke huko, tuangalie kwamba namna gani tuangalie kanchi kadogo kama Indonesia. Indonesia hawana resources kabisa, natural resources lakini wamewekeza kwenye skills za watu wao kiasi kwamba wameweza kukuza uchumi wao kwa hali ya juu sana kuliko kutegemea mikopo au misaada. Misaada inatudumaza, misaada inatufanya kwamba kila tukikaa unasema wawekezaji au wahisani hawajatupa fedha, sasa matokeo yake nchi ambayo tuna utajiri mkubwa kama sisi Tanzania kwa nini tu-rely kwa donors kila wakati tunakuwa ombaomba. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia katika Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje. Kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Waziri Kivuli kwa hotuba yake nzuri aliyoitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, mimi naomba nizamie katika diplomasia ya kiuchumi. Naona nchi yetu tumeongelea hili tangu 2001 mpaka leo na inaelekea hata Mabalozi wetu hawajui katika diplomasia kiuchumi wanatakiwa wafanye nini. Tunaongea juu juu tu hatuzamii kusema diplomasia ya kiuchumi maana yake ni nini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua Waziri ni mwanadiplomasia sana lakini nasikitika kusema hotuba yake yote au sehemu kubwa imeenda katika mambo ya kisiasa kwa maana na diplomasia ya kiisiasa. Kwanza tuanzie karibu hapa nyumbani katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, inasikitisha sana kuona Wabunge wetu wa Afrika Mashariki hawajui wanaripoti kwa nani au wako chini ya nani? Je wako chini ya Bunge hili au wako chini ya Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi hawana hata ofisi. Sasa unampaje mtu jukumu kubwa kuitwa Mbunge wa Jumuiya ya Afrika Mashariki lakini hana hata Ofisi nyumbani kwake. Nchi ndogo kama Burundi wana ofisi za Wabunge wao wa Afrika Mashariki hata Rwanda na Kenya lakini Tanzania hatuna. Hii inaonesha jinsi Tanzania ambavyo tunachukulia mambo yetu kwa urahisi rahisi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hebu tuangalie, angalia shilingi yetu ya Tanzania na shilingi ya Kenya. Mpaka jana shilingi yetu ishirini na mbili ya Tanzania ndiyo unapata shilingi moja ya Kenya. Hivi wenzetu wametuzidi nini na tunazungumzia diplomasia ya kiuchumi. Mabalozi wetu wa East Africa wanajifunza nini au wanatuambia kwa nini wenzetu Kenya wanapiga hatua? Wakenya wako mbali sana angalia supermarket tu hata iliyoko Dar es Salaam, Mkenya ndiyo anaiendesha hata Kenya Commercial Bank, Tanzania Kenya tuna nini, Uganda tuna nini na Rwanda tuna nini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ninachoshangaa kama tunazungumzia mambo ya diplomasia kiuchumi, nakumbuka Awamu ya Pili kule Saudia walieleza kwamba wanataka mbuzi wengi kwa vile watu wakienda Hija wanatumia sana nyama ya mbuzi. Watu wakaja hapa (Waarabu), Ubalozi wetu sijui ulifanya kazi yoyote kufuatilia suala lile lakini foreign officers wakapigapiga ikaishia hapo. Sasa hivi wenzetu wa Comoro ndiyo wanapeleka Uarabuni ng‟ombe na mbuzi kutoka Tanzania. Tunaongelea diplomasia ya kiuchumi, uko wapi uchumi wetu tunaouzungumzia hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie wawekezaji, wanakuja wawekezaji sijui Foreign Ministry yetu inasaidiaje kuonyesha hawa wawekezaji kule kwao wana uwezo kiasi gani ili waweze kutushauri kwamba hao muwakubali kama wawekezaji au msiwakubali? Unakuta wawekezaji wengine wanakuja kukopa kwenye benki zetu hizi hizi, halafu unaambiwa ni mwekezaji huyu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi angalieni migodi yetu wageni kutoka nje wametawala migodi yetu Watanzania tunabakia kufanya kazi za vibarua. Wizara yetu ingeshauri kwamba hawa wawekezaji labda tuwape position moja, mbili hizi nyingine zote zibanwe na Watanzania. Watanzania mali yetu (contribution) yetu iwe ardhi yetu na wale wawekezaji waje na hela ili tuwe equal partners. Leo tunaongelea uchumi wa kidiplomasia lakini migodi yetu watu wetu ni kupigwa risasi kila siku na wageni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, angalieni hoteli zetu mfano Hoteli ya Serena na iliyokuwa inaitwa Kilimanjaro sijui sasa hivi imeshabadilishwa jina au bado.
Haya Hyatt. Hawa wenzetu wanapewa grace period kwamba msilipe kodi muangalie kwanza biashara, miaka mitano wakimaliza wanabadilisha jina leo Sheraton, kesho Serena sijui keshokutwa wataitwa nani? Tumekaa kimya, hiyo diplomasia kweli ya uchumi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie wawekezaji wanapewa umiliki wa mashamba kwa muda wa miaka 99, mwananchi sisi mpaka na watoto wetu hamna atakayekaa kushuhudia mkataba umeisha, tunawapa wawekezaji. Huko nchi za nje, je, kuna Mtanzania anakwenda apewe ardhi miaka 99? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshangaa kwamba tumejivunia tunaletewa msaada wa pikipiki na Wachina, jamani juzi sijui miaka kumi iliyopita tuliletewa baiskeli wanakuja ku-assemble pikipiki kiwanda chetu cha jeshi pale Nyumbu ambacho kilikuwa kinatengeneza magari pale Kibaha, kingeombewa hela wangekuwa mbali siye tunarudi kwenye pikipiki. Pikipiki zitabeba mizigo gani, ndiyo diplomasia ya uwekezaji huo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu vyuo vya ufundi, tumeenda kuomba hela, wakati nafanya Danish Embassy tulitengeneza Chuo cha Chang‟ombe na Dodoma kwa grant leo tunaenda kuomba mikopo kurudi tena kutafuta technical assistance kutoka nje. Tunajivunia Italia wanatusaidia, hivi Engineers wetu wote kutoka chuo kikuu kutoka iliyokuwa technical college wameshindwa kusaidia kutengeneza VETA kweli mpaka twende tukaombe huko Italia? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba USD milioni 55 kujenga maghala, maghala mangapi tunayo yamewekwa uchafu hayawekwi hata mazao? Leo tunaomba USD milioni 55 msaada wa kujenga maghala, hivi kweli hata kujenga maghala jamani tushindwe nchi hii? Wenzetu wanatengeneza ndege wako mbali sisi bado tunatafuta msaada wa kujenga maghala? Hii diplomasia ya kwamba tuna marafiki siyo urafiki siye ni ombaomba, hakuna urafiki na ombaomba. Ukiwa na rafiki kila siku yuko mlangoni kwako anaomba utasema huyo ni rafiki yangu siyo rafiki. Tumekuwa nchi ya ombaomba hata vile vitu tunavyoweza kutengeneza wenyewe, inatuaibisha sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii. Mengi yameshasemwa, lakini napenda ni-concentrate katika mambo mawili au matatu. La kwanza, nilikuwa naangalia ripoti hii ya wenzetu, ni nzuri sana, Kamati inawapa pongezi mmeiweka ripoti vizuri. Nilipokuwa napitia ukurasa wa 42 kuhusu ukuaji wa Sekta ya Kilimo na kwamba asilimia 70 ya nchi yetu wananchi wetu wanategemea kilimo na kwamba sekta hii ndiyo inaweza kuondoa umaskini hasa vijijini na kweli vijijini ndio kwenye hii asilimia kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikaanza kujiuliza, hii slogan ya Kilimo Kwanza tumeisikia muda mrefu sana, slogan hii sikuona ikiwekewa mikakati ya jinsi ambavyo ingeweza kutekelezwa. Nilikuwa nikipitia, nikiangalia jinsi ambavyo Kilimo Kwanza kingetekelezwa wakati kila sekta inafanya bajeti yake, Sekta ya Maji imegeukia kulia, Sekta ya Kilimo imegeukia kushoto na sisi tunaongelea Kilimo Kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama priority ilikuwa katika umwagiliaji, kwa akili ya kawaida ungetegemea hizi sekta mbili ziweze kufanya assessment, ni maeneo gani basi tunakwenda kuyaboresha, je, tunakwenda kwenye Bonde la Rufiji, kulikojaa maji, yale maji tunayatoaje pale? Ili bonde lile liweze kuilisha Tanzania na nchi za jirani, hilo hulioni. Hiyo slogan imekwisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuja slogan ya viwanda nayo naiangalia, hivi priority ya viwanda vyetu ni ipi, tunaangalia vyuma au tunaangalia kilimo ambacho tunajua kwanza ndiyo uti wa mgongo ili tuwe na ile backward and forward linkage tuweze kuoanisha kwamba kama basi tunataka viwanda priority yetu iko kwenye moja, mbili, tatu. Kwa hiyo, wakulima wetu wawezeshwe katika kilimo hiki na pesa nyingi iwekwe hapo, hasa katika umwagiliaji na ninyi muangalie ili tusitegemee mvua, huvioni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, najiuliza hivi viwanda navyo vitakuwa kama Kilimo Kwanza, nchi yetu kwenda kwa slogans tu? Kama tunakwenda kwa slogans hivi tunamdanganya nani. Ningetegemea basi hata Wizara hii ya Fedha na Mipango waite hizi sekta Ministries wakae pamoja wawe focused, waangalie kwamba tunaomba pesa nyingi iwekwe katika sekta hizi mbili, tatu, ili tuweze kupata azma tuweze kufikia lengo letu la viwanda, kinyume cha hapo hii slogan nayo itapita kama ilivyopita ya Kilimo Kwanza. I am sure ukiangalia unaona kilimo kimewekwa pembeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Kamati wametuwekea vizuri sana kwamba hii sekta itategemea umwagiliaji, sasa kama umwagiliaji Wizara ya Maji na Umwagiliaji wameweka mikakati ya kufanya sensa kwamba ni sehemu gani kuna maji mengi yanayoweza kutumika kwa umwagiliaji ili iweze ku-demarcate yale maeneo kwamba yatamwagiliwa na kwa malengo gani, kwamba tuta-produce kiasi gani? Nilishangaa wakati mmoja, nafikiri ilikuwa mwaka jana, Waziri wa Kilimo alivyozungumza, alipokuwa Soko la Kibaigwa kwamba ameshangaa mazao yamekuwa mengi sana na storage hamna, kwa hiyo yapo nje yananyeshewa yanaharibika, Waziri wa Kilimo anashangaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu tunasema tuna upungufu wa chakula, kwa kweli ukiangalia ni utani, ingekuwa hizi Wizara zinaendeshwa na Wapare na Wachaga ningesema hawa ni watani wa jadi, lakini unaona watu tuko serious, tunakaa hapa Waziri anasema ameshangaa mavuno ni mengi hamna pa kuweka, hii inaniambia kwamba hatufanyi kazi kwa kuweka malengo au malengo yetu tunaweka madogo sana, hatuwi realistic, hatutumii wataalam wetu kufanya projections, matokeo yake tunashangaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachonishangaza zaidi, wakulima na wafugaji wote wako chini ya Wizara moja na kila siku kuna vita kati ya wakulima na wafugaji. Hivi hiki Kilimo Kwanza ambacho sasa Kamati hii inatilia mkazo kitakuwaje kama mtu amelima kesho ukiamka wanyama wameingia wamekula mazao yako yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unaangalia Wizara moja mmeshindwa kuja na mikakati ya kuona mifugo yetu itunzweje, kilimo chetu kitunzweje. Bado wafugaji wetu ni wale wa kuswaga, zile artificial insemination centers zimekufa wakati ukiangalia hizi Sekta za Kilimo, Ufugaji na Utalii zingeweza kutoa nchi hii katika umasikini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunaambiwa tuna ng‟ombe wengi, viangalie ving‟ombe vyetu vilivyokondeana, uliza anatoa lita ngapi per day, tunaringa katika Afrika Tanzania ni ya pili ikifuatiwa na Ethiopia, yet miaka yote hii hatuna mikakati. Unamwambia mfugaji punguza mifugo humpi target, huyu anafuga 2,000, huyu 10,000, huyu 500, huyu 200, unamwambia apunguze, apunguze kutoka wapi kwenda wapi, akipunguza anapeleka wapi, kama anamuuzia Mheshimiwa Profesa Maghembe ni palepale si ndiyo, mifugo inatoka hapa inakwenda pale, hatuna viwanda vya nyama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa anapunguza anapeleka wapi, unatoa mzigo kichwani unaweka begani ndiyo kupunguza huko? Kibaya zaidi humpi alternative, unaboreshaje ng‟ombe wako, tuwe na shamba darasa weka ng‟ombe kumi tukuonyeshe jinsi ya kuwaboresha vis-a-vis ng‟ombe wako 1,000, mfugaji ataweza kuelewa. Hufanyi hivyo unamwambia punguza, amuuzie nani, kiwanda kiko wapi?
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Sasa nasema kwa kweli kama nchi yetu inge-concentrate Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa anapunguza anapeleka wapi, unatoa mzigo kichwani unaweka begani ndiyo kupunguza huko? Kibaya zaidi humpi alternative, unaboreshaje ng‟ombe wako, tuwe na shamba darasa weka ng‟ombe kumi tukuonyeshe jinsi ya kuwaboresha vis-a-vis ng‟ombe wako 1,000, mfugaji ataweza kuelewa. Hufanyi hivyo unamwambia punguza, amuuzie nani, kiwanda kiko wapi?
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Sasa nasema kwa kweli kama nchi yetu inge-concentrate na kilimo tungekwenda mbali sana. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Na mimi niungane na wenzangu kutoa pole sana kwa wafiwa wote waliofiwa na watoto wetu wale waliofariki kule Arusha kwa ile ajali.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nielekeze mchango wangu katika upande wa umwagiliaji maana najua hapa ndio kwenye maisha yetu Watanzania wote. Ukiangalia tafiti ambazo zimefanyika za REPOA na ESRF zote zimeonesha kwamba, Tanzania kama tunataka kutoka katika umaskini lazima msisitizo uwe katika kilimo cha umwagiliaji, kama hatukuweka msisitizo katika kilimo cha umwagiliaji hata tukitengeneza barabara kiasi gani tutakuwa tunajidanganya, maana nchi ambayo haiwezi kujilisha haina heshima yoyote hapa duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia hata Jarida la Economist la 2012 linatueleza jinsi ambavyo Tanzania ni nchi ya kumi na moja duniani ya kuwa na maji mengi ambayo ni maji yale tunasema maji ya baridi au maji ambayo hayana chumvi. Ukiangalia Ziwa Tanganyika peke yake lina asilimia 17 ya maji yote masafi katika ulimwengu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ukiweka na Mito ya Pangani, Rufiji na Maziwa mengine tuliyonayo hakika utajua kwamba Tanzania tuna utajiri mkubwa sana wa maji. Licha ya maji tuna mabonde makubwa sana yanayofaa kwa umwagiliaji. Tafiti pia zimeonesha na Mheshimiwa Waziri amezungumza, kwamba tuna mabonde hekta milioni 29.4 yanayofaa kwa umwagiliaji. Lakini inasikitisha kwamba mpaka sasa ni hekta 468 tu ambazo zimejengewa miundombinu, na hiyo ni kama asilimia mbili tu ya sehemu yote ambayo imejengewa miundombinu ya umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunauliza hivi kweli Watanzania tunatakaje kuondokana na umaskini wakati hatutilii mkazo zile sekta ambazo zitatutoa kwenye umaskini? Unaangalia unajua je, ni kwamba hatutaki kutumia akili zetu tuko tayari tukaombe misaada kutoka nje, tukachukue misaada kutoka nje? Tungekuwa kama nchi za huko Ethiopia, Sudan, hivi nchi hii si tungekuwa tumeshakufa wote. Kwa hiyo, ninachosema, ni kwamba nchi yetu bado hatujatumia busara, hekima na akili Mungu alizotupa kwa ajili ya kuona vipaumbele vyetu viwe katika nini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kilimo kwa mwaka 2010 kilikua kwa asilimia 2.7 lakini mwaka jana kimeshuka hadi asilimia 1.7, tatizo unaambiwa uhaba wa mvua, ni aibu. Maji yamejaa tunazungumzia uhaba wa mvua kwa nini akili zetu zote tunapeleka kwenye mvua? Haya mambo ya kilimo cha umwagiliaji tumezungumza miaka nenda, rudi tangu kilimo kwanza, lakini mpaka leo tuna tatizo hilo, sijui tusemeje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukija Jimbo la Same Mashariki Mungu ametujalia tuna mito mikubwa ukichukulia Nakombo, Hingilili, Saseni, Yongoma lakini mito yote hii inakwenda baharini, mito yote inapita kwenye vichaka. Tumeomba tujengewe mabwawa ili akinamama ambao wengi ndio wanaolima wapate nafuu, akinamama ndio watekaji maji wengi ndio wanahangaika. Watoto wetu wa shule wako wengine boarding wanafuata maji kilometa nzima au mbili, ugonjwa wa UTI haupungui kwenye boarding schools, ugonjwa wa kuharisha watoto, akinamama kila siku wako hospitali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba bajeti ya Wizara ya Afya iongezwe. Tunasema hapa Wizara ya Afya iongezewe pesa kumbe yote inaenda kutibu kuharisha, matumbo, kwa nini tusingeboresha maji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nasema, nchi yetu tukiendelea kwa mtindo huu, tusipojali maji na hasa tuseme maji ya kumwagilia akina mama, mboga mboga, akina baba mashamba, vijana wetu hasa kule Jimbo la Same Mashariki kilimo cha tangawizi ambapo LAPF wanataka wajenge kiwanda kikubwa, hakiwezi kufanya kazi kama tangawizi haitapata maji ya umwagiliaji. Kwa hiyo naomba wenzetu walione hilo tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishuke kuangalia nini kinachotufanya Tanzania tunarudi nyuma. Hata tukisema bajeti ya Wizara ya Maji iongezwe, ambavyo naunga mkono, je, ubadhirifu ambao uko katika Wizara ya Maji nao tutaufanya nini? Ukiangalia ukaguzi wa ufanisi wa ujenzi wa miradi ya maji hasa ya mijini kwa mwaka 2010/2011 na mwaka 2013/2014 imeonesha katika miradi tisa, miradi nane iliongeza gharama zake kuanzia asilimia 10 mpaka asilimia 229 sawa na ongezeko la shilingi bilioni 30. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa je, Wizara ikiongezewa bajeti sasa hivi itatuhakikishiaje kwamba haya maji yatawafikia hasa akina mama ambao katika Tanzania wako asilimia 51 na na kati yao asilimia 60 wako vijijini? Tupunguze bajeti ya kwenda huko kwenye miji ili asilimia 30 iende mjini, 70 iende vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nasisitiza kwamba tungeanzisha Wakala wa Maji Vijijini badala ya Mfuko wa Maji ili tuwe na uhakika maji kweli yanaenda vijijini na kwamba maji yatawafikia wananchi vijijini. Kinyume cha hapo fedha itawekwa kwenye mfuko halafu hela zitakwenda ndivyo sivyo. Kwa hiyo, ningeomba sana, hata kama tukisema tunaweka umeme mwingi, barabara za lami kama akina mama vijijini watakuwa wanahangaika na maji, hakika nchi hii hatutaendelea. Akina mama ndio wenye uchumi mkubwa katika nchi hii, ndio wakulima wadogo wadogo. Tume-fail katika mambo mengi lakini hebu tuwape akinamama chance, tupeleke maji vijijini, tuanzishe huu Wakala wa Maji Vijijini ili tuwe na hakika hela kweli inaingia huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishie hapo.
Ahsante.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti ya Benki ya Dunia katika uzinduzi wa Ripoti ya Kumi ya Mwenendo wa Uchumi Tanzania imeonesha wazi kwamba katika nusu ya kwanza ya mwaka huu wa 2017, uchumi umeshuka kutoka 7.7% hadi 6.8% ukilinganisha na kipindi kama hicho mwaka jana (2016). Ripoti hii inanipa wasiwasi juu ya jinsi mpango huu unaoandaliwa utakavyotekelezwa kama mapato yetu ya ndani yatapungua siku hadi siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari zetu (TPA) hasa ya Dar es Salaam mizigo imepungua sana kutokana na ongezeko la tozo kwa mizigo iendayo nchi za jirani pamoja na mifumo mibovu ya bandari yetu. TPA imeshindwa kuboresha mifumo na miundombinu yake kutokana na kwamba mapato yake yanapokusanywa na TRA yanapelekwa kwenye Consolidated Fund Account na ama hayarudishwi au yanarudishwa baada ya muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri wakati atakapojibu hoja za Waheshimiwa Wabunge aeleze kama fedha/mapato ya wharfage ya TPA yanarudishwa kwa wakati au Mheshimiwa Waziri anaweka time frame ya mapato hayo kurudishwa TPA. Vinginevyo bila modernization ya TPA, wateja wengi watapitishia mizigo yao Durban, Beira au Maputo na matokeo yake bandari itakufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kilimo cha umwagiliaji, napenda kuunga mkono kwamba fedha zitengwe za kutosha katika sekta ya kilimo, hasa kilimo cha umwagiliaji, kilimo cha kutegemea mvua kimeongeza umaskini kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sekta za mifugo na uvuvi; nchi yetu inajivunia sana kuwa na mifugo wengi, ikiwa ni ya pili Barani Afrika baada ya Ethiopia. Mifugo inaweza kubadilisha sana kiwango cha maisha ya wafugaji kama mkazo utawekwa katika ufugaji wa kisasa. Ufugaji una faida nyingi licha ya nyama na maziwa, ngozi yake inaweza kuliingizia Taifa fedha nyingi. Serikali pia inashauriwa kudhibiti kwa uingizaji wa nyavu ndogo badala ya kuzichoma na hivyo kuongeza kiwango cha umaskini kwa wavuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Benki ya Wanawake na Benki ya Kilimo, benki hizi mbili zingeweza kuchochea maendeleo ya wananchi wa kima cha chini. Bahati mbaya Serikali na BOT wameshindwa kuisimamia Benki ya Wanawake na hivyo mtaji wake kushuka chini ya kiwango kinachokubalika kisheria. Serikali pia imeshindwa kutimiza ahadi zake za kuiongezea Benki ya Kilimo mtaji kama ilivyoahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, out of Tshs. 800 billion ambazo Serikali ilikuwa iipatie TADB, ni Tshs. 60 billion tu ambazo kati ya hizo, ni Tshs. 10 billion tu za kukopesha tangu mwaka 2015, mpango ulikuwa TADB ipatiwe Tshs. 10 billion kila mwaka. Hii undercapitalization ya benki hii itaifanya isiweze kukopesha wakulima na hivyo kilimo kuzorota.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kati ya hizo Tshs. 10 billion, ni Tshs. 2 billion tu ndiyo wamekopeshwa wakulima. Fedha nyingine zimekopeshwa benki nyingine. Katika kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge, naomba Mheshimiwa Waziri alieleze Bunge kwamba atahakikishaje TADB inaongezewa mtaji wa Tshs. 10 billion kila mwaka na jinsi Mheshimiwa Waziri anavyoweza kuisimamia benki hii ili fedha ziwafikie wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu umeme wa vijijini (REA), viwanda haviwezi kuanzishwa bila kupeleka umeme kwenye vijiji. Pamoja na kuanzishwa kwa Rural Energy Fund, TANESCO wameshindwa kuwasilisha fedha, kiasi cha Tshs. 7.4 billion kwa Mfuko wa REA zitokanazo na levy pamoja na faini ya ucheleweshaji. Ni vyema Mheshimiwa Waziri wa Fedha atueleze kwa nini TANESCO hailipi deni hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashirika ambayo Mpango huu katika ukurasa wa 48 unalenga kuyaimarisha na kuyatumia katika kuleta mageuzi ya viwanda nchini, ni vizuri Mheshimiwa Waziri akayaangalia upya kama watumishi waliopo wanaweza kwenda na kasi ya Sera ya Viwanda. Kwa mfano SIDO, STAMICO, CARMATEC na COSTECH wana rekodi ambazo si nzuri kiutendaji. Mheshimiwa Waziri atuhakikishie kwamba taasisi/mashirika haya yana wafanyakazi wenye ujuzi, waadilifu au uwezo wa kwenda na kasi ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, SIDO wameacha kilio kikubwa sana kwa wakulima wa tangawizi Wilayani Same. Tangu mwaka 2012 wametengeneza mashine za kuchakata tangawizi ambayo haijafanya kazi hadi sasa, hivyo kuwatia hasara kubwa sana wakulima. CARMATEC wana maeneo mengi waliyopewa kazi ya kutengeneza mitambo ya biogas na uvunaji wa maji, lakini hawakukamilisha kazi hizo pamoja na kulipwa fedha zote. COSTECH walipewa kazi ya ushauri na NIDA na kazi yao haikutumika hata baada ya kulipwa fedha nyingi; ina maana ushauri wao haukukidhi mahitaji ya NIDA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu matumizi mabaya ya fedha za umma, katika kipindi kinachoishia Juni, 2016, kati ya mapendekezo 3,898 yaliyotolewa na CAG, ni mapendekezo 1,449 tu (37%) yaliyotekelezwa kikamilifu. Hata zile Wizara zilizobainika kutumia fedha vibaya zilizopitishwa kwenye bajeti, bado Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameendelea kuwaongezea fedha kwenye bajeti. Nimuombe Mheshimiwa Waziri atoe mapendekezo jinsi atakavyoweza kuweka mpango madhubuti wa kuhakikisha mapendekezo ya CAG yanafanyiwa kazi kwa ukamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusus suala la kutozingatiwa sheria ya manunuzi na mikataba mibovu. Serikali imekuwa inapoteza fedha nyingi kutokana na Wizara na taasisi zao kutozingatia Sheria ya Manunuzi, kuingia mikataba mibovu na kushindwa kuwalipa wakandarasi kwa muda wa makubaliano. Matokeo yake Serikali inapoteza fedha nyingi zikiwemo za kulipa faini. Fedha hizo zingetumika katika kuleta maendeleo. Waziri alihakikishie Bunge jinsi Wizara yake itakavyosimamia jambo hili kuzuia upotevu wa fedha za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo hapo juu, naamini yatasaidia katika kuboresha Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2018/2019.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuunga mkono taarifa hii ya Kamati, naomba kutoa yangu katika kusisitiza haya yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kuhusu kilimo cha matuta. Bado Serikali haijasimamia vya kutosha kilimo cha matuta kwenye sehemu za miinuko ili kuzuia upoteaji wa maji na mmomonyoko wa udongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni matumizi ya mito. Serikali haijafanya juhudi kubwa kuweka ramani ya mito yote tuliyonayo Tanzania na kuona jinsi inavyoweza kutumiwa kikamilifu. Kwa mfano, Jimbo la Same Mashariki tuna mito mikubwa minne, lakini mito yote inaenda baharini na wakati huo huo inapita porini bila kunufaisha wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi nimeuliza maswali Bungeni pamoja na kuandika barua Wizara ya Maji na Umwagiliaji nikiomba Jimboni kwangu mito hiyo itengenezewe miundombinu ya mabwawa ya kukusanya maji na ya umwagiliaji. Wizara imelifumbia macho jambo hili. Je, usalama wa chakula utapatikana wapi kama hatutilii maanani kilimo cha umwagiliaji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia maji ya Jimboni kwangu kutoka mito hiyo tajwa hayajatumiwa kikamilifu kwa ajili ya kupelekwa katika Mbuga ya Wanyama ya Mkomazi. Maji hayo yangeweza kupelekwa kwa njia ya mtiririko (gravity flow), badala yake wanachimba visima ambavyo baada ya muda mfupi mabwawa hayo hukauka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ufugaji wa kisasa. Ufugaji bado umeendelea kuwa wa kienyeji sana. Ningeshauri Serikali ianzishe Mashamba Darasa sehemu za wafugaji ili kuonesha ufugaji bora unatakiwa uweje. Jimboni kwangu wafugaji walitenga maeneo ili wafundishwe jinsi ya ufugaji wa kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Serikali kukubali kuwa wangeanzisha Shamba Darasa hilo ni takribani miaka miwili sasa bado Serikali haijaweza kusaidia wafugaji hao. Inasikitisha kila mara Serikali inawataka wafugaji wapunguze mifugo bila kuweka idadi ya juu sana inayokubalika kwamba mfugaji mmoja anatakiwa kuwa na mifugo mingapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ubovu wa barabara za vijijini. Kilimo hakiwezi kuwa na tija kama barabara za vijijini hazikuboreshwa kutokana na ubovu wa barabara hizo. Wakulima wengi huuzia mazao yao mashambani na hivyo kupata bei ndogo sana. Hivyo, naunga mkono hoja kwamba bila barabara nzuri, bila maji ya umwagiliaji na bila kuwa na mifugo iliyoboreshwa nchi yetu haitaondokana na umaskini kwani uchumi wetu unategemea sana hizo sekta tajwa hapo juu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie machache juu ya Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji.

Kwanza nitoe pole kwa Wizara hii nyeti sana kwa kuwa wanapewa fedha kidogo sana kwa ajili ya kusambaza maji. Kwa sababu hiyo, naomba kupendekeza kuwa Serikali ichukue hatua madhubuti ya kutenga fedha angalau si chini ya asilimia 60 ili kuondoa tatizo kubwa linalowakabili wananchi wengi hapa Tanzania. Nchi haiwezi kuwa ya uchumi wa kati wa viwanda kama hata maji nchi imeshindwa kupelekea wananchi wake. Ni wazi kwamba ukosefu wa maji unasababisha magonjwa ya milipuko na hivyo kuongeza matatizo ya wagonjwa kujazana hospitali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili naishauri Wizara ya Maji na Umwagiliaji ianze kuweka takwimu sahihi za vyanzo vya maji ili ianze kuyatumia kikamilifu kabla ya kuchimba visima ambavyo baada ya muda mfupi vinakauka. Jimbo la Same Mashariki lina maji mengi ya mito, lakini maji yote yanaelekea baharini badala ya kupelekwa kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kuchukua nafasi hii kuishukuru Serikali kwa kuona umuhimu wa kufanya uamuzi mzuri wa kutenga fedha za upembuzi yakinifu na usanifu wa Bwawa la Yongoma. Mradi huu wa Bwawa la Yongoma utaweza kuinua uchumi kwa kiwango kikubwa katika vijiji vikubwa vya Ndungu, Misufini, Kalemawe na Makokane. Naamini baada ya upembuzi huu na usanifu mradi utatengewa fedha ili tupunguze matatizo ya maji kwenye Jimbo la Same Mashariki. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Kilimo. Watanzania wote tunakubaliana kwamba zaidi ya asilimia 60 ya wananchi hupata ajira zao kupitia sekta ya kilimo. Pia tunakubaliana kwamba sekta hii hutoa chakula chote cha wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha ni kwamba kilimo hapa nchini kinachukuliwa kama cha kujikimu tu na wala hakuna mpango mkakati wa kuonesha kwamba kilimo chetu kimejiandaa kufanya biashara ya kuhakikisha tunauza mazao kwa wingi nchi za nje ili kuongeza fedha za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kilimo chetu kinategemea mvua kwa kiasi kikubwa. Katika ukurasa wa saba wa hotuba ya Waziri ameonesha kuwa mwaka 2016/2017 uzalishaji ulipungua kutokana na uhaba wa mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna dhamira ya kufanya kilimo cha umwagiliaji, Wizara itafanikiwaje kama Idara ya Umwagiliaji bado iko chini ya Wizara ya Maji? Nashauri Waziri alete pendekezo Bungeni kusema kwamba Idara ya Umwagiliaji ihamishiwe Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Same Mashariki lina mito mingi na ardhi zaidi ya hekta 300,000 ambazo zinafaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Nimeomba Wizara ya Maji tusaidiwe miundombinu ya umwagiliaji. Ni mwaka wa tatu huu maji ya mito yote yanaenda baharini na Wizara haikujali hata kujibu kama wana mpango gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Kilimo amesema kuwa mazao ya kilimo huchangia asilimia 65 ya malighafi yanayohitajika viwandani. Je, kumekuwa na mkakati gani kati ya Wizara hizi mbili kuona jinsi zitakavyoshirikiana ili kuhakikisha ni viwanda gani vitawekwa mikoa gani ili kuwe na hakika ya uzalishaji wa mazao hayo kutosheleza mahitaji ya kiwanda tarajiwa? Kwa mfano, Wilaya ya Same imechagua zao la tangawizi kuwa ndilo litatumiwa kuanzisha kiwanda kikubwa cha kuchakata tangawizi. Pia kuna tarajio la kutoa tangawizi nyingi ili kiwanda kiweze kuzalisha kwa soko la nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la wazi ni kwamba tangawizi inahitaji maji mengi sana. Tatizo ni kwamba hakuna miundombinu ya umwagiliaji ya kutosheleza kupanua kilimo hicho. Wakati LAPF wanawekeza kujenga kiwanda kikubwa na kuweka mashine za kisasa, je, malighafi za kutosha zitapatikanaje wakati hakuna miundombinu ya umwagiliaji? Naomba Waziri wa Kilimo aeleze kwamba kilimo kitakuwaje bila umwagiliaji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo la Maafisa Ugani kwamba huko vijijini na kwenye kata hawasaidii wakulima. Waziri akihitimisha hotuba yake aeleze jinsi Wizara yake itakavyoweza kufanya kazi na TAMISEMI ili kuwaondoa Maafisa Ugani ambao hawana tija na kisha kuajiri na kusimamia utendaji kazi wa hawa Maafisa Ugani kwenye vijiji, kata na kwenye wilaya. Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Mwaka wa 2017/2018. Nataka kujikita katika maeneo machache na hasa nikiangalia maeneo ya kipaumbele katika mwaka huu wa 2017/2018. Viko vinne, lakini nitataja viwili tu. Kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa uchumi wa viwanda, hiyo nakubali; kufunganisha uchumi na maendeleo ya watu; hapo ndipo ninapoona tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mahali ambapo kuna wananchi wengi ambao ndiyo wanataka focus yetu iangalie ni vijijini kwenye sekta kubwa inayoajiri wananchi wengi, ambayo ni Sekta ya Kilimo. Nilikuwa najiuliza, hivi bila kuweka kipaumbele katika kilimo, mifugo na uvuvi, tunafunganishaje uchumi na maendeleo ya watu? Kwani watu wengi wako katika sekta hiyo ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mwaka huu unaoishia 2016/2017, kilimo kilipata shilingi bilioni 3.369 sawa na asilimia 3.31; mifugo na uvuvi walipata shilingi bilioni 1.2 sawa na asilimia nane tu ya fedha iliyoidhinishwa na Bunge. Sasa tunaposema kilimo ndiyo uti wa mgongo wa nchi yetu ambao inachangia asilimia 28 katika maendeleo ya nchi yetu, Iweje basi asilimia 96.69 haikuidhinishwa, badala yake wamepewa asilimia 3.3 tu? Hivi kweli Sekta hii ya viwanda itakuaje kama hatuunganishi na malighafi kutoka kwenye kilimo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naona kwamba mambo yetu yako mismatch kwamba hatu-focus kwamba kama kweli tunataka viwanda na kama tunataka kuondoa umaskini, lazima concentration yetu iwe katika kilimo, ambapo kule ndiyo kuna wananchi wengi. Kule ndiko kuna maskini wengi na kwa ajili hiyo tukiongeza thamani kwenye mazao yao, kwenye viwanda tutakuwa tumewasaidia wananchi wetu kwa sehemu kubwa katika kuondoa umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia sekta nyingine ya Wizara ya Maliasili na Utalii, hii ni Sekta ambayo pia inachangia asilimia 25 (mnaweza kunisahihisha) katika uchumi wetu. Nayo ilipewa shilingi milioni 156.6 sawa na asilimia nane ya fedha walizoomba. Sasa hii ina maana kwamba asilimia 92 ya pesa yote waliyoomba hawakupata. Sasa ninachojiuliza, kama hata Sekta hii ya Utalii ambapo Balozi wa Marekani aliyekuwa Black American wakati ule hapa nchini, alisema, Tanzania hii kwa utalii wake tu kama wangeweka emphasis kwenye utalii, sisi tungetoka Marekani kuja kuomba msaada katika nchi hii. Sisi tunapuuzia zile sehemu ambazo ndizo zinachangia katika uchumi wetu kukua haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli kuweka barabara na reli ni kitu kizuri na ninakiunga mkono, lakini tuwe focused kwamba reli inaenda kuchukua nini kwa mfano Mwanza? Je, kilimo cha pamba tumekitilia mkazo? Je, viwanda vinavyowekwa ni vya kutengeneza nguo ili tuongeze thamani katika pamba zile au tunaweka huku kiwanda, usafiri unawekwa pengine na maji yanawekwa pengine? Sasa huu uchumi wetu wa Tanzania na huu umasikini tunauondoaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, najiuliza, maajabu gani tutakayopata sasa hivi kwenye kodi ambayo tutatoka kwenye ile shilingi trilioni 29 tuingie shilingi trilioni 31.7? Tunakusanya vitu gani? Pesa zinatoka wapi? Ukiangalia, hata hii tunayosema tuchukue kodi ya nyumba ambazo hata hazikuthaminiwa, kwa kweli ni maajabu sana. Kwanza itakuwa ni kilio kikubwa kwa wananchi wetu maskini, kwamba juu ya shida walizonazo vijijini, bado tuwaongezee mzigo ambao wanatakiwa walipe Sh.10,000/= kwa kibanda cha mbavu za mbwa! Hii kweli mimi siioni ni sawa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitegemea kwamba aidha bajeti yetu ibaki ile ile, tu- address ule upungufu wote ambao kwa mwaka huu unaoisha hatukuweza kuufikia au ipungue ili tuwe very realistic, tuseme kwamba tutafanya kazi kwa pesa ambayo tunayo. Mfadhili akileta itakuwa bonus. Sisi tuna-assume kwamba hawa wafadhili watatuletea tu au tutapata mikopo as a result tunaweka bajeti kubwa ambayo mwisho wa siku tunarudi kusema ooh, bajeti ya maendeleo ilitekelezwa kwa asilimia
38. Ni aibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, tukiingia kwenye hii kodi ya mafuta ya taa, kwa kweli mimi hili siliungi mkono kabisa. Mafuta ya taa ndiyo nishati kubwa sana vijijini, especially ukingalia kwa mama zetu wengi ndio wapishi, wengi hasa wa mjini pia, wanatumia haya majiko ya kichina ambayo yanatumia mafuta ya taa. Sasa hivi hapa kwenye Bunge lako tunaambiwa mkaa unakatazwa, kuni zinakatazwa, tusikate miti; kuna mwenzetu alisema sasa hivi tunaleta gesi. Hivi ana habari gesi hii miaka saba mpaka kumi ijayo ndiyo itaweza kuingia majumbani kwetu kwa kutumia mitungi? Ana habari hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hawa akinamama maskini vijijini, wakae miaka saba mpaka kumi wakingojea gesi? Mimi nafikiri hii kodi ya mafuta ya taa tuiondoe ili wanawake wengi ambao ndio wapishi; vibatari huko vijijini ndiyo vinatumia mafuta ya taa, tuwasamehe katika kuongeza hiyo Sh.40/= kwenye mafuta ya taa. Kwa hiyo, nasema kama hii bajeti kweli inajali maskini, nasema hii Sh.40/= itolewe kwenye mafuta ya taa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maji. Nashauri ianzishwe agency ya maji vijijini, maana tumeshaona pesa nyingi za maji zinakwenda kwenye maji ya mijini na kutokana na audit report ya CAG imeshaonesha kwamba kuna ubadhirifu mkubwa sana katika hii miradi ya maji ya mijini. Kwa hiyo, sioni kwa nini maji bado yaendelee kuwekwa mjini badala ya kupelekwa vijijini. Kwa hiyo, nashauri kwamba angalau asilimia 70 ya bajeti ya maji ipelekwe vijijini ili kusudi akinamama tuwatue ndoo vichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira, kweli hii inashangaza sana. Kama hatutatilia mkazo ajira na ukiangalia standard za ILO, tuzungumzie gainful employment, tusizungumzie tu ajira, maana ajira tunaambiwa mbona mashambani watu wanaajiriwa wengi, ardhi yetu ni kubwa! Tuangalie gainful employment, watu wapate kipato kutokana na ajira zile. Hapa katika mpango huu sioni mahali ajira ilipowekewa msisitizo. Kwa maana hiyo ni kwamba, tutatoa wanafunzi wengi wanaomaliza Vyuo Vikuu, wanamaliza VETA na maeneo mbalimbali ambao watakuwa mijini. Katika uzee wetu tutakuta wanatuingilia mpaka majumbani. Tunatengeneza majambazi wengi ambao kesho hatutaishi kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema kabisa tungeangalia kwamba ajira zetu tunaziwekaje ili tuone tuna- create vipi ajira hii? Hii kusema kila mtu aanzishe viwanda, hiyo siyo practical. Viwanda vina systems zake, siyo kwamba mimi kila leo nikiamka naenda kuanzisha kiwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza uangalie mtaji unapata wapi? Kiwanda cha aina gani? Hata hicho kiwanda ukianzisha ume-import material. Vipuri unatoa wapi? Soko lako liko wapi? Ni kitu kikubwa ambacho kingetakiwa Serikali ibainishe yale maeneo muhimu ambayo tunasema tukianzisha kiwanda hiki, kitaajiri wananchi wangapi na material yake yatatokana na kilimo, tuta-add value na tuta- export wapi ili tupate ajira na tupate fedha kwa ajili ya kuendeshea shughuli zetu za maendeleo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nasema bado sijaridhika kwamba uchumi wetu… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Nasikitika sauti yangu kidogo siyo nzuri nilikuwa na flu lakini nisameheni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita katika mambo mawili, matatu hivi. La kwanza nitaangalia hii kaulimbiu ya awamu ya tano kuhusu viwanda, lakini pia nitaangalia jinsi ambavyo Serikali inajipanga kuwekeza katika kuboresha miundombinu ambayo itasaidia viwanda hivi viweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika taarifa ya Waziri Mkuu amesema kwamba hadi kufikia Februari, 2018 viwanda vipya 3,306 vilikuwa vimeanzishwa. Nasema wazo la kuanzisha viwanda ni zuri maana nia ni kuboresha nchi yetu kufikia katika uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo langu kubwa ni jinsi ya utekelezaji wa hii miundombinu. Rais alivyotamka hilo kama ndiyo kipaumbele chake nilitegemea kuwe na mkakati madhubuti ambapo sekta mbalimbali zinakaa, Wizara zinakaa kuangalia kwenye kila Mkoa kuna opportunity gani za kuanzisha kiwanda gani. Katika hizo kuangaliwe miundombinu imeboreshwa? Je, kuna barabara za kwenda sehemu iliyotengwa kuwekwa hicho kiwanda? Je, kuna maji? Je, kuna umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu nachokiona hapa ni kwamba imefika hatua Tanzania sasa hivi tunafanya kazi kama maroboti. Inatamkwa watu wanakimbia, tunapata sifa kwamba tumeanzisha vitu hivi, je, tunaangalia sustainability yake au tunajua kuanzisha tu? Je, tumejifunza vile viwanda vyote vilivyokufa viliuawa na nini? Je, kutokana na hapo tunajiwekaje vizuri ili hivi tunavyoanzisha visije navyo vikafa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa vile nina mfano mdogo tu, Kamati yangu ya PAC ilivyokuwa inatembelea viwanda mbalimbali nilipata shock kidogo nilivyofika kwenye Kiwanda cha Kibaha cha Kutengeneza Matrekta. Matrekta yale yamejazana pale ndani hayana soko na ukiuliza hakuna mtu anayejua hawa wanaotengeneza matrekta haya kutoka nchi za nje chini ya Wizara wamejitangazaje, yanajulikana au kuna mahali ambapo yamefanyiwa hata testing ili kuangalia ubora wake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema Mkoa wa Pwani una viwanda vingi, nafikiri hata hiki cha trekta kimewekwa lakini yamejazana ndani mle, hayafanyi kazi, hayajafanyiwa testing kuonesha kama yanahimili ardhi za kwetu. Kibaya zaidi ni kwamba hata watu kufundishwa bado hawajafundishwa ku-assemble tunategemea hao wenzetu kutoka nje, Wazungu ndiyo tunapanga mkakati wa kupeleka wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uone nchi yetu tunavyofanyakazi upside down kwamba Mkuu wa Nchi ametamka watu wote wanakimbia hatukai tukafaya analysis, kwanza tuka-evaluate huko nyuma tulikotoka tulikosea wapi na mkoa gani uko endowed kuweza kufanya kitu ambacho kweli kitakuwa productive kwenye nchi yetu kikawekewa miundombinu yote ili uchumi wetu ukaanza kukua kupitia pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalia matrekta ya Suma JKT huko yalikopelekwa. Kwanza hayajulikani yamepelekwa wapi which means hata Wizara ya Kilimo hawajatathmini matrekta haya ya Suma yaliyokopeshwa watu mbalimbali yamewezaje kuboresha kilimo badala yake tunaona kilimo ambavyo kimeanguka, mwaka hadi mwaka kilimo kinaanguka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna dawa hizi za kuua viluwiluwi vya mbu na dawa hii inatengenezwa Kibaha, tumefika pale maboksi kwa maboksi yamejazana. Wakalalamika kwamba Halmashauri nyingi walishapelekewa au walishakopeshwa lakini ni kama moja au mbili ambazo zimelipa nyingine zote hazijalipa. Waheshimia Wabunge tuliokuwa nao wakasema kwenye Majimbo yao au Wilaya zao hawajui kama hata hiyo dawa ipo wala hawajui Halmashauri hizo walishachukua hizo dawa. Maana yake ni kwamba zimewekwa hapo Halmashauri, hazitumiki kuua viluwiluwi vile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dawa zile wanasema vile viluwiluwi vikishaota mabawa dawa ile haiwauwi, kwa hiyo inawauwa kwenye septic tanks yale maji machafu sasa imagine huko vijijijni wangapi wana hayo matenki ya maji machafu, wengine vyoo vyao viko pembeni pembeni huko. Kuna wenzangu ambao vyoo vyao bado ni kwenye migomba, sasa sijui hiyo dawa au hicho kiwanda kitakuwa sustained kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninachosema with due respect napenda sana tuijenge nchi yetu maana hii nchi ya watu wote, lakini kama tunafanya vitu kwa pupa, talk of numbers siyo quality, hatutafika popote. Tutakuwa na viwanda 10,000 au milioni but at the end of the day tunaweza kuona kwamba return ya zile investments ni zero. Sasa viwanda kama hivyo tunavi-sustain namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nitoe mfano kidogo tu kule kwenye Jimbo langu la Same Mashariki kuna Kiwanda cha Tangawizi. Kiwanda hiki sitatoa historia yake lakini nipende tu kusema LAPF wameungana na wakulima, wamechukua asilimia 60 ya ownership na wakulima asilimia 40, well and good. LAPF wamefikia hatua sasa hivi wanataka ku-install mashine kubwa, wameshapitia michakato yote ili kiwanda kianze kazi, sheshe linakuja barabara kwanza ya kutoka Mkomazi kwenda Same imekuwa historia miaka nenda rudi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii inatumiwa na wananchi wa Majimbo kama manne au matano ya Korogwe Vijijini, Mlalo, sehemu ya Lushoto, Same Mashariki na Same Magharibi. Barabara hii tumepiga kelele miaka nenda rudi. Kilichonishangaza mwaka 2015/2016, Wizara ya Miundombinu ilisema imetenga pesa ambayo ilikuwa shilingi milioni 145 kwanza kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa Mkomazi – Kisiwani - Same, hizo zilikuwa pesa za bajeti ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Barabara ulitenga shilingi milioni 450 kwa ajili pia hiyo hiyo ya usanifu wa kina wa barabara hiyo, total ni shilingi 595 milioni kwa ajili ya usanifu huo, lakini mpaka leo hakuna hata kilometa moja ambayo imetengezwa. Sasa unajiuliza hivi hiki Kiwanda cha Tangawizi ambacho Mfuko huu wa Jamii wa LAPF wanataka waanze na ilikuwa waanze soon mwezi huu watapita wapi? Ukiangalia hata wakulima wenyewe miundombinu ya maji hawajatengenezewa, hiyo production ya kiwanda kikubwa watapata malighafi kutoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Kwa vile nina dakika tano tu, naomba niende straight kwenye points zangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme ukweli kwamba namheshimu sana Waziri Mheshimiwa Profesa Mbarawa, Waziri wa Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Naomba tu kuongezea facts ambazo alitoa Mheshimiwa Kitandula, Mbunge wa Mkinga alipoanza kuzungumzia juu ya barabara ya Same – Kisiwani - Mkomazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Mbarawa ajue kwamba barabara hii ina umuhimu wa kipekee. Kwanza ilikuwa barabara ambayo iko kwenye Great North Road ikafanyiwa magumashi ikabadilishwa kwa sababu ambazo sitazitaja hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande huu wa Same Mashariki una hazina kubwa sana ya utajiri mkubwa sana wa maji, mvua, mazao na barabara hii inatumiwa na wakazi wa Korogwe Vijijini akiwepo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali anakaa sehemu hiyo; inatumiwa na wenzetu Jimbo la Mkinga aliko Mheshimiwa Kitandula; inatumiwa na wakazi wa Mlalo, Jimbo la Mheshimiwa Shangazi; inatumiwa na Same Magharibi kwa Mheshimiwa Mathayo; na inatumiwa na Same Mashariki kwa Mheshimiwa Naghenjwa Kaboyoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa haya yote Mheshimiwa Waziri ajue ana National Park ambayo Faru mweusi alitolewa kutoka Czech akaletwa akawekwa pale Mkomazi National Park ili watu wengi waweze kwenda kumwona. Akumbuke kwamba kuna mradi mkubwa unajengwa na LAPF ambapo tangawizi yake itatoka kwenye haya Majimbo yote ya hawa Waheshimiwa niliowataja. Akumbuke kwamba nilishasema hapa na Mheshimiwa Spika aka-join akisema katika Mkoa wa Kilimanjaro ni Jimbo la Same Mashariki tu ambalo halina barabara ya lami iliyokamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi mkubwa ambao UNCDF - Capital Development Fund wanakuja kuwekeza katika kupandikiza samaki ambapo kuna bwawa ambalo lilitengenezwa tangu Wakoloni walipohamisha wananchi kutoka Mkomazi National Park, wakawatengenezea hili bwawa ambalo lina ukubwa wa 24 square kilometers.

Mheshimiwa Mwenyekiti, UN Secretary General anaye-deal na UNCDF Deputy ali-fly kutoka New York alikuja KIA kuangalia sehemu ule mradi utakapowekwa, akatia tick. Akasema huu utakuwa ni mradi mzuri sana ambao utapandikiza samaki wa kisasa kutoka South America ambao wataweza kuwa ndio kitovu cha kusaidia Tanzania kupata samaki wa hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo mafupi namwomba Profesa Mbarawa, ametengea Jimbo hili au barabara hii Sh.265,000,000 kwa kilomita 96.5, lakini hapo hapo upembuzi yakinifu uliofanywa mwaka 2015/2016 ulitumia Sh.595,000,000 kufanya huu upembuzi yakinifu. Mwaka 2016/2017 ulishafanywa tena upembuzi yakinifu; Mwaka 2017/2018 nimeambiwa juzi na Meneja wa TANROADS kwamba pia walipita kufanya upembuzi yakinifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikuwa napiga kelele hapa kwa ajili ya barabara hii nikijua Mheshimiwa Mbarawa anajua umuhimu wa hii barabara ndiyo maana mara tatu unafanyiwa upembuzi yakinifu, ambapo najua gharama zake zitakuwa imefika shilingi bilioni moja. Sasa kama anafanyia barabara, upembuzi yakinifu na upembuzi wa kina kwa kutumia zaidi ya shilingi bilioni moja, lakini atoe shilingi milioni 200 na kitu, kweli hii?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, naomba nichangie machache katika hotuba ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Same Mashariki lina wafugaji wengi ambao bado wanafuga kienyeji. Wafugaji hawa walishatenga eneo kubwa kwa ajili ya kufanyiwa shamba darasa la jinsi ya kufuga kisasa na kupanda majani ya mifugo. Wilaya ya Same ina eneo takribani ekari 300,000 ambalo linafaa kwa ufugaji. Hivyo naomba Waziri awaeleze wananchi wa Jimbo la Same Mashariki, ni lini wataalam watafika jimboni hapo kuanzisha shamba darasa? Jambo hili nimeshapeleka ombi kwenye Wizara hii na Mheshimiwa Naibu Waziri Ole-Nasha alifika jimboni humu mwaka jana, lakini akashindwa kuwatembelea wafugaji hawa waliokuwa wamejiandaa sana kuonana naye.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili Jimboni Same Mashariki kuna bwawa kubwa lenye eneo la kilometa za mraba 24. Ziwa hili limejaa udongo na hivyo hata samaki hawawezi kuzaliana.

Mheshimiwa Spika, UNCDF walikuwa tayari kuanzisha mradi mkubwa kwa kutumia cages. Maandalizi yote yalikwishafanyika pamoja na kuweka muundo wa PPP, Halmashauri ya Wilaya ya Same ikishiriki kikamilifu. Lakini kutokana na tatizo hili la tope kujaa bwawani, wafadhili wanajaribu kuona jinsi ya kutengeneza mabwawa ya samaki nje ya Bwawa hili la Kalemawe lililoko Kata ya Kalemawe, Same Mashariki.

Mheshimiwa Spika, kwa vile Mito ya Hingilili na Yongoma inatiririsha maji yake kwenye hili Bwawa la Kalemawe, kutolitumia ni hasara kubwa kwa nchi yetu maana matokeo yake bwawa hili litakufa.

Naomba Waziri akihitimisha hoja yake anieleze jinsi atakavyoweza kusaidia ili bwawa hili lenye samaki linaweza likatolewe tope ili liweze kuleta kiwanda cha kuchakata samaki. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa mchango wangu kwa Wizara hii kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Same Mashariki lina tatizo kubwa sana la usafirishwaji wa mazao pamoja na abiria. Jimbo la Same Mashariki limebarikiwa sana kuwa na mito mingi pamoja na mvua za kutosha. Kwa hiyo, wananchi wanalima sana mpunga, tangawizi, mahindi na ndizi. Pato kubwa la Halmashauri ya Same yanatoka Jimbo la Same Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Same - Kisiwani - Mkomazi ndiyo ilikuwa barabara kuu kutoka Nairobi – Arusha - Dar es salaam, yaani ilikuwa The great North Road. Kutokana na siasa za wakati wa miaka ya 1970’s zilizokuwa zinaendeshwa Wilayani Same (wakati huo ikiwa ni Wilaya moja na Wilaya ya Mwanga) ilisababishwa kuanzishwa barabara ya lami ya sasa kutoka Dar es Salaam kupitia Mkomazi – Bwiko – Hedaru – Makanya – Same – Moshi
– Arusha, matokeo yake wananchi wa Same, Kisiwani, Maore, Ndungu, Kihurio, Bendera, Mkomazi wakawa-cut off, maana usafiri wa mabasi uligeuza njia na kupitia njia mpya. Hili lilisababisha umaskini mkubwa kwa wananchi wa sehemu hii ya Same Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa kuna miradi mikubwa ya Kitaifa inayoanzishwa Jimboni Same Mashariki. Miradi hii inaitikia wito wa Serikali wa kuanzisha viwanda. Miradi hiyo ni pamoja na LAPF, tayari wameagiza mashine ya kisasa ya kuchakata tangawizi. Tangawizi hii ina soko kubwa nchi za Uarabuni pamoja na Ulaya hasa Holland na Ufaransa. Wananchi kutoka Majimbo yanayopakana na Jimbo la Same Mashariki ambao pia wanatumia barabara hii ya Same Mashariki - Mkomazi yaani Majimbo ya Korogwe Vijijini, Mkinga, Mlalo na Same Magharibi ni kati ya wakulima wa Tangawizi ambao watafaidika na kiwanda hiki cha LAPF.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Umoja wa Mataifa (United Nations Capital Development Fund-UNCDF) wamemaliza mchakato wa uanzishwaji wa mabwawa ya kisasa ya uzalishaji wa samaki ambao watatosheleza mahitaji ya ndani ya nchi na pia kusafirisha nchi za jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi mkubwa wa umwagiliaji katika Kata ya Ndungu ambao uligharamiwa na Serikali ya Japan. Mradi huu unazalisha mpunga mwingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nimeleta hiyo background ili niiombe Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ifikirie upya kutenga fedha za kutosha ili hii barabara ya Same –Kisiwani - Mkomazi itengenezwe yote kwa kiwango cha lami. Kiuchumi itaongeza pato la Taifa na kuhakikisha sustainability ya viwanda vinavyoanzishwa. Fedha iliyotengwa kwa barabara hii ni kidogo sana kiasi impact yake haitaonekana kimaendeleo. Zaidi ya hivyo, ijulikane kwamba Jimbo hili la Same Mashariki limekuwa marginalized kwa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu iangaliwe fedha iliyotengwa kwa Mkoa wa Kilimanjaro na kiasi kinachopelekwa Jimbo la Same Mashariki utaona Jimbo hili halitengewi haki. Kibaya zaidi, kiwango cha kutengeneza barabara hizi mbili yaani Same – Kisiwani - Mkomazi ina kilometa 96.46 na Mwembe – Myamba - Ndungu kilometa 90 kimekuwa cha chini sana. Wamekuwa wakirudia rudia maeneo yale yale siku zote na kukwepa kutengeneza maeneo korofi. Sehemu kubwa haijengwi mifereji na hata Makaravati huwa yanakuwa yakifukiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hisia kubwa kwa wananchi wa Jimbo la Same Mashariki kwamba kuna mchezo mchafu pamoja na ufisadi unaoendelea katika utengenezaji wa barabara hizi, ndiyo maana naona hata fedha nyingi zinatengwa kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wakati hakuna mpango wa kutengeneza barabara hii ya Same - Kisiwani - Mkomazi kwa kiwango cha lami. Inawezekana fedha hizi zinatumika kwa manufaa ya watu wachache.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna sababu ya kupoteza fedha nyingi kwenye usanifu wakati hakuna nia ya kuiweka lami barabara hii ya Same – Kisiwani - Mkomazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia kuhusu miradi ya Kimkakati ya Mchuchuma na chuma na Liganga.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ieleze Umma kama ni kweli katika sehemu hii ya Liganga kuna aina ya madini (products) zinazojulikana kama Vanadium Pentioxide na Titanium ambayo vinatumika katika kutengeneza ndege kwa kuwa ni vyepesi (light) na hivyo kuwa na thamani kubwa ukilinganisha na Chuma? Pia, je, baada ya ku-extract madini haya, chuma kinaweza kuchukuliwa kama by product? Ni vyema jambo hili likaangaliwa kwa ukaribu zaidi ili nchi isije ikapoteza mali nyingi zinazotoka ardhini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Same, kuna madini mengi sana ya Jasi (Gypsum), maeneo ya Makanya na Bendera. Jasi huwa inatumika kutengenezea “POP” (Plaster of Paris), kutengenezea mabomba ya majitaka, ceiling boards, mbolea na sehemu nyingine inatumika kwenye Viwanda vya Saruji.

Mheshimiwa Naibu Spika, “Deposits” zilizoko maeneo tajwa hapo juu ni mengi kiasi kwamba kungeweza kuanzishwa viwanda takribani vinne hivi. Naishauri Wizara hii ya Viwanda, isaidie kutuma wataalamu maeneo haya ili kufanya uchunguzi juu ya deposits hizi za gypsum na uwezekano wa kuanzishwa viwanda hivyo kwa kushirikiana na Wizara ya Uwekezaji. Lengo ni kutekeleza Azma ya kuifanya Tanzania Nchi ya Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wa Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa scenarios tatu ambazo zinanifanya niwe na mashaka kwamba Wizara hii ya Kilimo itaweza kusaidia kupatikana kwa malighafi za kuingia kwenye viwanda. Najua kwamba Wizara hii inategemea Wizara nyingine ili waweze kufanikiwa, matokeo yake ni kwamba Wizara hii hata ingewezeshwa kiasi gani, kama haya matatizo ambayo nitayazungumzia hapa hayakuangaliwa, sioni itakavyoweza kusaidia kwamba asilimia 65 ya malighafi iingie kwenye viwanda vyake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, wananchi tunajua kwamba sasa hivi miwa imekomaa sana, iko mashambani, lakini inashindikana kupelekwa kwenye viwanda kwa tatizo la kwamba barabara hazipitiki. Kwa maana hiyo, ni kwamba wakati Serikali inajenga viwanda, wakati Serikali inawekeza katika mashamba makubwa ya miwa, Wizara ya Ujenzi haina habari kwamba kunatakiwa kuwe na barabara ya kutoa malighafi mashambani kufika viwandani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi viwanda vya sukari ambapo sukari ingekuwa iko nyingi sasa hivi nchini, haiwezi kutengenezwa kutokana na kwamba miwa hii inaozea shambani sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiuliza Serikali, kama hakuna jinsi ya kukaa pamoja na kuona tunawezaje kufanya sustainability ya hivi viwanda tunavyotaka kuanzisha, tutafanya nini ili basi tuweze kujikwamua? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie tunapopata ukame. Katika ukurasa wa namba saba, Mheshimiwa Waziri amesema mwaka 2016/2017 kumekuwa na ukame, kwa hiyo uzalishaji ukaanguka. Miaka yote tunazungumzia umwagiliaji, lakini ni wazi kwamba Idara ya Umwagiliaji iko Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Maji haina mpango wa kuona kwamba je, kuna mashamba gani makubwa ya uzalishaji ambayo yanatakiwa huu umwagiliaji ukafanywe kule? Imekuwa ni wimbo wa Taifa kila mwaka tunazungumzia Kilimo cha Umwagiliaji lakini matokeo yake, Wizara ya Kilimo inafanya vyake, Wizara ya Maji na Umwagiliaji inafanya vyake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija scenario ya tatu, ni kwamba wakati hali ya hewa inakuwa nzuri, production inakuwa kubwa kama tulivyoona kwenye mahindi na mbaazi, yamevunwa mavuno mengi. Tatizo, hatuna soko, haturuhusiwi kuuza nje. Sasa swali langu ni kwamba kukiwa na mvua nyingi, kuna mafuriko, mazao hayawezi kutoka kwenda viwandani, kukiwa na ukame hakuna maji ya kumwagilia kuweza kuzalisha mazao, kukiwa na hali nzuri wananchi wakazalisha sana hakuna jinsi ya kupata masoko ya kuuza hizi products. Sasa nauliza hivi hapa tunafanya ngonjera, utani au tuko really serious? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napata shida sana kwamba ni lipi bora kwetu? Kwenye mafuriko hatuangalii kwamba siku moja kutakuwa na mafuriko, kwa hiyo, mashamba kama ya miwa yatengenezewe structure ambazo zinaweza kutoa miwa mashambani kwenda kwenye viwanda. Matokeo yake tuko tayari tutoe pesa ya nchi hii ikaingize sukari kutoka nchi za nje kuliko kutengeneza miundombinu yetu. Sasa hapa sustainability na hivyo viwanda tunavijengaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, hii Idara ya Umwagiliaji, labda sijasoma vizuri, lakini sijaona mahali ambapo Mheshimiwa Waziri anapendekeza kwamba Idara hii ya Umwagiliaji kwa vile inakwenda kwenye kumwagilia mashamba, ihamishwe kutoka Wizara ya Maji iingie kwenye Wizara hii ya Kilimo ili wanapotengeneza mkakati wa kwamba ni mashamba gani yalimwe, basi ionekane kwamba maji yatakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii scenario ipo hata kule kwangu Jimbo la Same Mashariki. Tunaweka kiwanda sasa hivi kikubwa cha tangawizi, barabara hakuna, maji hakuna, lakini tuna-invest a lot of money kwa ajili ya kutengeneza hiki kiwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kweli tutaweza kumsaidia Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli afikie azma yake ya kuifanya nchi hii ya viwanda na uchumi wa kati kama kila Wizara inafanya contrary? Yaani hakuna complementarity, hakuna mawasiliano kwamba priorities ziende huku wakati wa kutengeneza barabara na wakati wa kutengeneza mashamba makubwa ya kumwagilia. Tunafanya kazi kwa compartments, kila mmoja anaangalia kwake na haangalii kwamba kweli huu uchumi tunaufikiaje kama tunataka kufikia uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niulize, hivi kwa mfano mbaazi, kwa nini tume-rely kwenye soko moja tu la India ?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie hotuba hii sehemu mbili; kwanza kwa kuwa vita vya Kagera historia yake haijawekwa vizuri ili vizazi vijavyo viweze kujua jinsi Jeshi letu la Ulinzi lilivyopigania nchi hii na kumwaga damu yao ili kutetea nchi yetu kutoka kwa Nduli Idd Amin, naomba kushauri kwamba historia ya vita hivi iandikwe na kuwekwa kwenye nyumba zetu za makumbusho na pia kwenye library za vyuo vyote vya elimu ya juu. Nakumbuka kazi hii ya uandishi iliashaanza na Mwenyekiti wake akiwa Spika Mstaafu, Pius Msekwa na Katibu wake alikuwa Luteni Kanali Livingstone Kaboyoka kwa vile hawa wote wawili wako bado hai ningeshauri mawasiliano yafanyike ili wasaidie kutoa taarifa muhimu ya vita hivi vya Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwa kuwa TARURA inafanyakazi za matengenezo ya barabara mijini na vijijini, ningeshauri Jeshi la Kujenga Taifa lisaidie kuunda vikosi vya vijana hasa vijijini wakiwapa mafunzo ya ukakamavu na kuwasaidia wapate mafunzo ya kutengeneza barabara hasa vijijini ili badala ya kutoa pesa nyingi kwa wakandarasi ambao wakiondoka wanaacha barabara zikiharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, JKT ingeweza kufanyakazi na TARURA na kuunda Road Building Brigades ambao wanatokana na maeneo husika. Hizi brigades zingeweza kupatiwa basic equipments kama sururu, majembe, mapanga, mabeleshi na wheelbarrows ili kila mara wakarabati maeneo wanamoishi. Malipo yao yanatokana na michango ya wananchi na magari/pikipiki zinazotumia barabara hizo. Tuna mifano Tanzania ambapo enzi za ukoloni kulikuwa na vituo vya matengenezo ya barabara kila maeneo ya barabara. Kambi hizo zilikuwa zinajulikana kama PWD. Ahsante
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa shukrani zangu kwa Serikali kwa kusaidia kukarabati miundombinu ya maji katika Jimbo la Same Mashariki, Kata ya Maore ambapo wanyama pori waliharibu miundombinu ya maji. TANAPA walitoa fedha kwa hiyo tatizo hili limetatuliwa.

Pili, pia nitoe shukrani zangu kwa TANAPA kwa ushirikiano mzuri walio nao kwa wakazi wanaopakana na Hifadhi ya Mkomazi. Baada ya kusema hayo naomba nitoe changamoto zinazowakabili wananchi waishio karibu na hifadhi hii ya Mkomazi, nazo ni hizi:-

(i) Kutokana na kwamba Hifadhi ya Mkomazi haina maji ya kutosheleza kwa ajili ya hawa wanyamapori, wanyama hawa bado wanatoka kwenye hifadhi na kwenda kufuata maji kwa wanavijiji. Kwa maana hiyo miundombinu hiyo iliyokarabatiwa hivi karibuni iko hatarini kuharibiwa tena.

Mheshimiwa Spika, kwamba TANAPA watenge fedha ili wachukue maji ya mtiririko (gravity water) kutoka chanzo cha Mto Hingilili ambao una maji mengi na hayajawahi kukauka tangu kuumbwa kwa dunia hii, chanzo hiki cha Mto Hingilili alisha kwenda kukiona Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA Mr. Kijazi na kuahidi kutenga fedha kwa ajili ya mradi huu.

Mheshimiwa Spika, ni wazi kwamba Serikali inapoteza fedha nyingi kuchimba mabwawa ambayo baada ya muda mfupi maji yake hukauka na hivyo kusababisha wanyama pori kuvamia makazi ya watu. Wakati wanyamapori hawa wakienda kutafuta maji, huleta madhara makubwa kwa kula mazao ya wakulima pamoja na kujeruhi watu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kwamba mpaka wa Hifadhi hii ya Mkomazi umesogezwa karibu sana na makazi ya watu hasa wafugaji, kumetokea migogoro mikubwa kati ya TANAPA na wakulima na wafugaji. Tatizo ni kwamba wananchi hawakushirikishwa wakati wa kuweka mipaka. Matokeo yake ni kwamba wananchi wameachwa na ardhi kidogo wakati TANAPA wamechukua ardhi kubwa zaidi. Wananchi wanaona Serikali yao inathamini wanyama pori zaidi kuliko inavyothamini binadamu. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Same Mashariki wanaoishi karibu na Hifadhi ya Mkomazi, tunaomba mipaka iangaliwe upya ili wananchi watengewe eneo kubwa la malisho pamoja na eneo la kulima.

Mheshimiwa Spika, ni wazi kwamba barabara ya Same - Kisiwani - Mkomazi ambayo inapita kando kando ya Hifadhi ya Mkomazi, ni mbaya sana kiasi kwamba hata watalii hawawezi kuvutiwa kwenda kuona wanyama kwenye hifadhi hii. Itakumbukwa kwamba faru mweusi kutoka Czech alipelekwa kwenye Hifadhi hii ya Mkomazi. Hivyo basi TANAPA wana kila sababu kutafuta namna ya kuongea na Wizara ya Ujenzi ili barabara hii itengenezwe kwa kiwango cha lami ili kuweka mazingira mazuri ya kuvutia watalii kutembelea hifadhi hii. Ni wazi kwamba utalii ni sekta ambayo inaweza kuongeza pato la Taifa kwa kiwango kikubwa sana. Nchi zinazowekeza kwenye utalii uchumi wake ni mkubwa sana.

Hivyo sekta hii ni muhimu sana kwa ukuaji wa uchumi wa Tanzania ili tufikie azma ya kufikia uchumi wa kati, kati ya miaka ya 2025 – 2030. Hifadhi ya Mkomazi ina wanyama wa kila aina wakiwepo tembo, nyati, twiga na kadhalika. Hivyo naamini Wizara hii ya Maliasili na Utalii itaiangalia Hifadhi ya Mkomazi kwa jicho la tatu.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
Azimio la Kufuta Hasara itokanayo na Maduhuli ya Madeni ya Nyuma ya Ada na Leseni za Magari, Riba na Adhabu kwa kipindi kinachoishia tarehe 30 Juni, 2019
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende tu kusema kwamba kama Mheshimiwa Godbless Lema alivyosema kwamba Serikali imeanza lini kuwa tabia nzuri, naona hii itakuwa ni mwendelezo wa tabia nzuri. Niseme tu kwa kifupi kwamba, kuna maeneo mengine kwenye magari ya Serikali mengi ambayo yamekaa hayajaletwa kufutwa hapa yanaozea kwenye yards.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna dawa ziko kwenye bohari zetu ambazo zime-expire hazijaletwa. Kwa hiyo nimshauri tu Mheshimiwa Waziri kwamba wafanyie kazi ili walete mapema yale maeneo yote ambayo CAG amezungumzia ambayo hawajaleta kwenye Bunge yafutwe ili hoja zisiendelee kujirudia rudia. Ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii ili nami niweze kuchangia hoja ya kumpongeza Rais wa Tano aliyepita kwa njia ya kifo na Rais mpya wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwape pole wafiwa wote wa Tanzania na hasa wenzetu wa Chama cha Mapinduzi ambao wamempoteza kiongozi wao wa Chama. Naungana na Watanzania wote wanawake kwamba wanawake wamefurahi sana kwamba wamepata kiongozi mwanamke ambaye atapandisha hadhi ya wanawake; kunyanyaswa kwa wanawake tunajua sasa basi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upole, kwa hekima aliyonayo Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na kwa CV ambayo tumeiona, tunaamini kwamba atasimama katika nafasi yake kuifanya Tanzania iheshimike katika Taifa hili na nje ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, Watanzania wengi wanaamini kwamba kwa hekima yake atarudisha demokrasia kwenye vyama vyote vya kisiasa vipate nafasi kama ambavyo Muasisi wa Taifa hili Mwalimu Nyerere alitaka kwamba viwe na uhuru ambao ni kikatiba pia, kufanya mikutano yao bila kubughudhiwa na vyombo vya dola. Pia Watanzania wengi wanajua kuwa kupitia Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan uhuru wa Vyombo vya Habari na uhuru wa wananchi kujieleza utapatikana yeye akiwa ni mama mwenye busara na hekima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona hata Angela Merkel wa Ujerumani jinsi alivyopeleka ile nchi mpaka ikaheshimika mpaka leo. Tunajua kwamba nchi yetu ili iwe na upendo wa kweli na amani ya kweli ni lazima haki itendeke. Haki ndiyo inayoweza kuzaa amani ya kweli na kuleta upendo na umoja katika nchi yetu. Kwa hiyo, tunaamini kwamba kupitia mama kama ambavyo mmesifu, akinamama ni watu ambao hawana ubaguzi; hatujasikia hata siku moja mama akisema mwanawe akafanye DNA, maana watoto wote ni wake. Kwa hiyo, tunajua kwamba vyama vyote ni vyake, wananchi wote ni wake, wenye vyama na wasio na vyama ni wake. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, atasimama katika nafasi yake kuonyesha akinamama ambavyo tunaweza kuendesha nchi na isiingie kwenye mitafaruku wala vita. Kwa hiyo, tunashukuru na tunaamini kwamba Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan atalitendea Taifa hili kazi kubwa na ataonekana mwanamke wa kwanza siyo Barani Afrika tu na duniani kwamba nchi yetu hii ameipaisha kwa kurudisha demokrasia ya kweli, kurudisha vyama vyote viwe na nafasi sawa na kwamba akinamama wa Tanzania hawanyanyaswi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwombea Mwenyezi Mungu ambariki aweze kufanya kazi yake hii akiongozwa na Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia kidogo katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijatoa mchango wangu kwa ujumla naomba tu nizungumze kidogo kuhusu sheria iliyounda mawakala ikiwepo TANROADS maana nitazamia kwenye TANROADS. Kifungu namba 12(2)(a) cha Sheria ya Wakala wa Serikali Na. 30 ya mwaka 1997 kinataka wakala wote wafanye kazi kibiashara na mapato yao yatoshe kulipia matumizi yao. Hii sheria imetekelezwa kwa kiwango kidogo sana. Kwa mwaka 2015/2016, mapato ya ndani ya mawakala wengi yalishuka kutoka asilimia 45 hadi kufikia asilimia 16 mwaka 2020. Ni mawakala wachache tu walioweza kujitegemea, lakini mawakala wengi ikiwemo TANROADS wametegemea Serikali kwa kiwango cha asilimia 84.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka Waziri atakapokuja kuhitimisha atueleze tatizo ni nini ambalo linafanya Wakala wa Barabara TANROADS wasiweze kujitegemea angalau kwa kiwango kikubwa. Kama tatizo ni sharia, basi sheria iangaliwe upya, lakini kama si sheria tuambiwe tatizo ni nini. Pia TANROADS kwa mwaka uliopita unaoishia Juni walikuwa na deni la bilioni 833 na kati ya hizo bilioni 57 ni riba ambayo inatokana kutowalipa wakandarasi kwa wakati. Tatizo hili siyo la TANROADS, ni Wizara ya Fedha ambayo imeshindwa kuwapelekea hela kwa wakati, matokeo yake TANROADS wanadaiwa na wakandarasi kiasi kwamba ukiangalia riba ya bilioni 57 ni kubwa sana kiasi ambacho ingeweza kutengeneza barabara nyingi. Kwa hiyo, niseme kwamba sisi tuiambie Serikali inakwamisha sana wakala hawa kufanya kazi, maana nia ya kuanzisha hawa Wakala ni ili kazi zetu ziende kwa tija, lakini unapowakwamisha inapelekea kuonesha kwamba mawakala hawa hawafanyi kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba niingie kwenye hoja yangu ambayo naongea kwa niaba ya Wabunge watano kuhusu barabara ya Same - Kisiwani – Mkomazi. Barabara hii ambayo inatumiwa na Mbunge wa Same Magharibi, Mheshimiwa Mathayo ambayo pia inatumiwa na Mbunge wa Mkinga, Mheshimiwa Kitandula; Mheshimiwa Mnzava wa Korogwe Vijijini; Mheshimiwa Shangazi wa Mlalo na mimi mwenyewe. Ni barabara ambayo ina tija sana kwa Taifa kama ingetengenezwa kwa kiwango cha lami. Ni muda mrefu sana barabara hii tumeipigia kelele, tangu nilipoingia mara ya kwanza. Imeshafanyiwa upembuzi yakinifu mara tatu na mpaka mara ya mwisho nimeongea na Engineer Mfugale ambaye anaheshimika Kitaifa na Kimataifa, akaniambia alikuwa katika hatua ya mwisho ya kufanya design.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha ajabu barabara hii imetengewa milioni 300 kwa kilomita moja. Sasa hebu angalia barabara ambayo inatumiwa na Wabunge watano, wanaume wanne na mwanamke mmoja; wa CCM wane na wa CHADEMA mmoja; Viongozi wa Kamati za Kudumu wawili, bado Waziri haoni umuhimu kwamba hii barabara inategemewa na wapiga kura wengi wanaotokana na majimbo haya matano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli nasema barabara yoyote ukiitengeneza, unaangalia kwamba ina manufaa gani kwanza kiuchumi because lazima kuwe na return to capital, return kwenye investment, hatutengenezi barabara tu kumfurahisha mtu, nimeshaona barabara nyingine inatengenezwa kutoka kata kwenda kata ikawekwa lami na ukiangalia ina-produce nini pale, inabeba watu wangapi. Nasema na ndiyo maana nimesema niangalie hii sheria ya kuunda mawakala ili tujue, je, tunafanya kazi kibiashara au tunafanya kazi kihasara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe, Tanzania tutokane na kufanya kazi kana kwamba sisi hatujali uchumi wetu, Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, anajali sana kwamba nchi hii ipige hatua, tuingie nchi ya viwanda, ya uchumi wa kati, lakini kwa mtindo huu unampa kabarabara kamoja kadogo yaani kilomita moja unaangalia tija yake ni nini.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kusema TANROADS wamejitahidi, lakini kuna barabara zimetengenezwa kwa kiwango cha kutisha kibaya mno, Kamati yangu ilitembelea barabara kutoka Dodoma kwenda Iringa, ilikabidhiwa miaka minne iliyopita, inatisha na nafikiri niliona kama imetengewa tena hela. Sasa kama barabara zetu kwa muda mfupi inaharibika inarudi kuanzia kutengeneza tena na hii iko katika Great North Road, lakini imetengenezwa kwa kiwango cha chini kiasi kwamba tunaonekana kwamba laissez-faire. Hivyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri tuangalie utengenezaji wa barabara zetu, ametoka kwenye Maji, ameletwa kwenye eneo lake la kujidai tunaomba aangalie sana wakandarasi alionao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama barabara zetu kwa muda mfupi zinaharibika inaanza kutengenezwa tena na hii iko katika Great North Road lakini imetengenezwa kiwango cha chini kiasi kwamba tunaonekana Watanzania ni laissez-faire. Naomba Mheshimiwa Waziri tuangalie utengenezaji wa barabara zetu. Mheshimiwa Waziri umetoka kwenye Wizara ya Maji umeletwa kwenye eneo lako la kujidai, tunaomba uangalie sana wakandarasi ulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimeona kule kwenye barabara hii ninayozungumzia ya Same - Kisiwani - Mkomazi mara nyingi inatengewa fedha ambayo mnaziita Upgrading DSD, labda mtanieleza maana yake, inatengewa hela lakini kila nikipita sijaona mahali ambapo pamefanyiwa upgrading hapo hapo hiyo DSD inatengewa hela. Kwa mfano, hiyo upgrading DSD shilingi milioni 175 na mwaka huu imetengewa shilingi milioni 200 lakini nikipita sioni mahali palipotengenezwa. Labda baada ye utanielimisha maana ya haya maneno ni nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kibaya zaidi unpaved roads zinatengewa hela nyingi sana, shilingi milioni 848, mwaka jana shilingi milioni mia nane sijui ishirini na ngapi, mwaka juzi shilingi milioni mia nane na kitu. Sasa najiuliza, hivi kwa nini upeleke hela nyingi kwenye kuparura barabara wakati hela hizo hizo ungeweza kusema uziongezee utengeneze barabara ya kiwango cha lami? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kuna mambo mengi ya kutafakari, muda wetu wa kuongea ni mdogo lakini nafikiri ifike mahali tufanye analysis kwamba hivi hizi barabara tunajenga kisiasa au tunajenga kiuchumi ili uchumi wetu upande? Tukijenga kiuchumi tutapata pesa kutokana na kusafirisha mazao ya kilimo na kusaidia sekta nyingine kama za afya na maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ambayo nairudiarudia imechezewa kwa muda mrefu sana. Najua haitengenezwi kwa kiwango cha lami, maana ni rahisi ku- trace lami inatengenezwaje lakini mkandarasi anapopita anaiparura tu barabara hii kwa miaka yote na kila mwaka shilingi milioni mia nane arobaini na kitu, kwa kweli nafikiri kuna aina ya ufisadi ndani yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Waziri atakapojumuisha anieleze kwa nini barabara hii moja inawekewa pesa nyingi kwenye unpaved road? I do not know utaita unpaved nini lakini kwenye laki unaweka kilomita 1, kwenye ku-upgrade unaweka nusu kilomita lakini kwa shilingi milioni 200, maana yake ni nini? Mimi napenda nijue haya yote na hii pia ingetusaidia kuangalia kwa nini barabara hii ya Same, Same ina-control 39% ya Mkoa wetu wa Kilimanjaro lakini ndiyo wilaya maskini kuliko wilaya zote za mkoa ule. Kwa hiyo, naomba barabara hii iangaliwe kwani Same ingesaidiwa ina sehemu kubwa ya ku-expand social economically hasa kwa upande wa kilimo lakini Same hiihii ndiyo imewekwa pembezoni …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Nishati. Kwanza nipende kusema kwamba naunga mkono hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani. Pia nitaanzia pale Mheshimiwa Mwijage alipoachia alipojaribu kulinganisha barabara na bomba la gesi hili ya kutoka Songas na kuja Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba kwanza ukiangalia mradi wowote unaotakiwa kuanzishwa lazima uangalie cost effectiveness yake. Kwa maana yake lazima unaangalia return to capital, sasa anachotaka kututumainisha Mheshimiwa Mwijage ni kwamba haijalishi kama mtambo huu wa gesi unazalisha full capacity ama unazalisha under capacity.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa gesi kutokana na ripoti ya CAG ambayo imetoka Machi, 2018, unakuta kwamba matumizi ya mtambo huu ni asilimia 24 tu ukilinganisha na installed capacity. Kwa maana yake ni kwamba kwa asilimia 76 matambo huu una-run under capacity, maana yake ni nini, maana yake ni kwamba huu mtambo unaleta hasara maana TPDC lazima iendelee ku- service mradi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukiangalia kama TPDC itandelea ku-service mtambo ambao hauzalishi maana yake nini, hapo hapo unganisha na TANESCO. TANESCO wanashindwa kulipa ankara za TPDC ambayo TPDC inaiuzia TANESCO gesi asilia kwa kuzalisha umeme wa Kinyerezi, Ubongo II, Symbion Power Plus. Ni wazi kwamba TPDC itashindwa kulipa mkopo wa Exim Bank ya China. Tumejua madhara ambayo wenzetu walioshindwa kulipa mikopo hii imekuwa ni nini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mkataba ule Kifungu Na.2 ni wazi kwamba TPDC watakaposhindwa kulipa mkopo ule, Exim Bank ya China itachukua huu mradi na ui- run na ukijua kwamba wenzetu wa China wana fedha za kumwaga ni kwamba wataufanya u-run kwenye full capacity, gesi yetu yote itakuwa inachukuliwa kwa Wachina na sisi tutakuwa tunabaki tukishangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kusema tu kwamba, TANESCO wanajitahidi sana, lakini pamoja na jitihada hizo wanakumbwa na matatizo mawili. Kwanza TANESCO wanakuwa controlled na EWURA, EWURA ndiyo wanaopanga bei. Waheshimiwa Wabunge, wewe angalia una product yako unauza, lakini ni mtu mwingine anakupangia bei unategemea hiyo biashara iende kwa namna gani. Kwa mfano, TANESCO wananunua umeme kwa shilingi 544.65 kwa unit na kuuza kwa shilingi 279.35, haihitaji kwenda Chuo Kikuu kuchukua economics kujua kwamba kwa njia hii tunaiua TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili Mashirika ya Umma hawalipi madeni kwa TANESCO, TANESCO inadai fedha nyingi sana kwa mashirika mbalimbali ya umma. Pamoja na Mheshimiwa Rais kusema kwamba wakatie


umeme yale mashirika ambayo hayalipi umeme, napenda nikuulize wewe ambaye unailaumu TANESCO. Kama ingekuwa wewe uambiwe ukatie umeme Muhimbili, kwa ubinadamu ungeweza kuikatia Muhimbili umeme? Kama huwezi ina maana gani, kwa nini Serikali isichukue jukumu la kulipia mashirika yale ambayo wanajua hayatengenezi faida na hayawezi kulipia umeme. Ni wazi kwamba Shirika la TANESCO, kama halitaweza kusaidiwa na Serikali ni wazi kwamba litakufa katika muda mfupi ujao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo napenda kusema pamoja na Waziri amesema kwamba TANESCO hawahitaji ruzuku, lakini tujue kwamba kama Mashirika ya Umma hayalipi na sina hakika kama Wizara yenyewe ya Nishati wameshalipa deni lake kwa TANESCO. Je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka kuipa ruzuku au kulipia yale mashirika ambayo yameshindwa kulipa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye REA namba tatu, kwanza niseme namshukuru Waziri amefanya jitihada sana kumpigia Meneja kwenye Jimbo langu kwamba waweke umeme kwenye vile vijiji alivyoahidi. Tulifanya ufunguzi wa mbwembwe wa Mkoa wa Kilimanjaro pale Mwanga, lakini unakuta sasa hivi kinachotokea REA wanapeleka nguzo wanaweka hapa halafu wanatoweka. Sasa wananchi wanaona hiki ni kiini macho au maana yake ni nini? Pia nipende kuuliza, kule kwangu Jimbo la Same Mashariki kuna mito mikubwa ambayo ina maporomoko ambayo tungeweza kutumia maji kuzalisha umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati yangu ya PAC ilipotembelea Arusha Technical College tuliona wanafunzi wale wanavyojaribu kuzalisha umeme lakini kwa kutumia laboratory na kutumia ndoo za maji. Kwa nini Serikali isisaidie vyuo kama hivi vikaenda kufanya majaribio au practical kwenye mito kama hii ambayo ina maporomoko na kwa ajili hiyo nisingemsumbua Waziri kwamba vijiji vyangu na vitongoji vyangu havina umeme. Kwa hiyo naomba kwanza akija kuhitimisha anieleze kwamba mpaka sasa hivi ule mkopo Exim Bank wa China umelipwa kwa asilimia ngapi. Pili, napenda anieleze kwamba kama hawataweza kushinikiza mashirika ya umma yakalipa yale madeni, wanategemeaje TANESCO iendelee ku-survive? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho napenda nizungumzie tu kwamba katika ajira, katika Sekta ya Mafuta na Gesi inasikitisha kuona kwamba kampuni za ndani ziliweza kupata sehemu ya manunuzi au ya ku-supply vitu kwa asilimia tisa tu. Makampuni yote ya nje ndiyo yamefaidi miradi inayoletwa Tanzania. Ukiangalia mafunzo katika sekta hii yamefanywa kwa asilimia 20 tu kwa maana hiyo ina maana kwamba hatuna personnel ya kuweza ku-run gesi zetu au mitambo hii ya gesi. Ukiangalia katika wataalam waliofundishwa au walioelimishwa mpaka sasa labda wawe wameongezwa wengine kutokana na ripoti ya CAG, ni asilimia sita tu ambayo katika Sekta ya Gesi na Mafuta wameweza kupata masomo ambayo ndiyo relevant kwenye hii sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunachotaka kusema, hivi Tanzania kwa nini sisi tunakumbatia mashirika ya nje hata kama mradi ume-provide kwamba mafunzo yafanyike, hayafanyiki. Matokeo yake watu wetu hawapati ajira, watu wetu hawafaidiki na fedha hizi ambayo ni mikopo kutoka nje ambayo italipwa na jasho la wananchi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Spika, kwanza mimi badala ya kumpa hongera wifi yangu, Mheshimiwa Prof. Ndalichako, namna pole maana najua hapa kabeba mzigo mzito sana ambao ndiyo roho ya nchi yetu; nakupa pole sana.

Mheshimiwa Spika, na wakati nikiangalia kwa nini tumefikia hapa tulipofikia kwamba wanafunzi wetu anamaliza mpaka chuo kikuu anatembea na briefcase ya certificate kutafuta kazi; tatizo liko wapi. Nikaona niangalie maeneo mawili; la kwanza nimeangalia tulipoacha ile – sijui tunaita sera au nini – Mwalimu Nyerere alituweka katika njia ya kufikiria kwamba uhuru na kazi na pili, elimu ya kujitegemea. Nakumbuka elimu ya kujitegemea miaka hiyo nikiwa sekondari tulikuwa na mashamba kama ulivyokuwa unasema, tunalima tunapata chakula cha shule, lakini sasa hayo tumeyaacha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nililoona tumekuwa donor dependent so much that hiyo imetulemaza. Hata Mheshimiwa wifi yangu Profesa akizungumza alitaja wafadhili au wadau wengi wanaotusaidia katika elimu yetu. Hii imetulemaza kiasi kwamba hatukutaka kujijengea njia ya kujitegemea wenyewe na kutafuta hela, badala yake tumetegemea sana wafadhili. Sehemu kubwa ya pesa ya maendeleo mfadhili asipoileta kwa wakati tunaanguka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapo natumia theory ya mtaalam mmoja Mmarekani anaitwa Ajzen na theory yake ya planned behavior, aliandika mwaka 1991. Alisema kwamba: “An individual attitude is shaped by subjective norms in the leaving environment and later such attitude forms intention within an individual and consequently this becomes a behavior”. Kwa Kiswahili ambacho labda siyo sahihi sana alisema: “Fikra ya mtu iliyojengwa na mazingira anayoishi humpelekea kuwa na nia ya kutenda kila kitu fulani na nia hiyo ikiendelezwa baada ya muda fulani hugeuka kuwa tabia”. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema hivyo? Sasa hivi tuliwajengea wanafunzi wetu kwamba akimaliza shule lazima aajiriwe, hiyo kuwatoka haijawa rahisi. Nataka tu-compare na nchi za wenzetu ambao walikuwa maskini au walikuwa wako nyuma wakati wakipata uhuru. Tanzania tukilinganisha na nchi ambayo ni ya China na Japan; nataka kuzitumia hizo maana najua hali zao zilikuwa duni wakati wakipata uhuru. Kwa mfano, tukipata uhuru sisi mwaka 61 China walikuwa wamepata uhuru wao mwaka 49 na Japan 51, tulipishana kama miaka kumi au kumi na miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia umri wa kuanzia masomo ya wanafunzi wao wa primary ni ile ile miaka sita kama sisi. Miundo yao ya elimu haijatofautiana sana na sisi, tunakuja kupishana sehemu moja au mbili. Sehemu moja uwiano wa walimu na mwanafunzi, hapo sasa hivi ndiyo tuna shida kubwa sana. Mwalimu mmoja wa Tanzania anakuwa na wanafunzi wengi kiasi kwamba hawezi kujua kila mwanafunzi ana karama gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Japan mwalimu mmoja anahudumia wanafunzi 16.1, China 16.43, hii ni ripoti ya UNICEF siyo yangu sisi ni 50.63. Pia wameonyesha katika ripoti yao, ni ya siku za nyuma kidogo inawezekana mambo yamebadilika, wameonyesha kwamba wanafunzi wanaofaulu kwenda sekondari kwa Tanzania ni asilimia 54, Japan ni asilimia 98.8 na kwa China 97. What does that mean? Ina maana wao kwa vile ni compulsory na wanatumia ile system yao ambayo tangu primary school lazima wawe na vipindi vya ufundi na ufundi ule wanapewa equipment (vitendea kazi) kwamba hawa-relay kwenye nadharia kama sisi instead wao wanafanya kwa vitendo na zile product wanazotengeneza zinakuwa na value zinaenda hata kuuzwa.

Mheshimiwa Spika, hawa wanafunzi wakifika form four wengine wanakwenda kwenye shule za ufundi na wengine wanaenda shule za sekondari. Kiasi kwamba kama hakuweza kwenda chuo kikuu ameshajenga msingi na anajua aende akafanye kazi gani maana amepata zile skills. Kwa hiyo, zile skills zinawafanya wajenge tabia ya kujitegemea tofauti na sisi tunajenga tabia ya kwenda kuajiriwa.

Mheshimiwa Spika, wenzangu walikuwa wanasema tuwe na Baraza la Taifa la Elimu, lakini nafikiri hapo tutakuwa tumeji-confine sana, labda tuwe tunasema think tank ya kuangalia mfumo wetu mzima ambao utakuwa na linkage na viwanda, kilimo na Hazina kuona kwamba huu uchumi wetu na hasa shule zetu tunazi-revamp namna gani kusudi tujenge ile tabia ya kujitegemea. Kinyume cha hapo tutasema hatuja-improve hiki na hiki lakini wakijengewa tabia ya kujitegemea na tangu mwanzo tunaweka vifaa vya kutosha kwenye zile karakana na mwanafunzi akifika form four ameshajua anataka kwenda wapi. Hawa wenzetu hata university wana-liaise na viwanda, wanafanya attachment, wanakwenda kuona tunaweza kui-improve vipi viwanda vyetu au viwanda vinaweza kusaidiaje wale wanafunzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa kwetu sasa hivi tunafanya kazi kwa mtazamo mmoja, kama ni elimu tume-drawn a line ni elimu, kilimo ni kilimo. Sijui kama kuna mahali ambapo tuna-converge, tukitaka kuanzisha kiwanda lazima tuangalie skills gani tunawapa wanafunzi wetu, kwa priority ipi na kwa viwanda vipi. Bila kuweka huo muelewano kwamba hawa wa viwanda wanajua priority ya viwanda vyetu ni hizi, kwa hiyo tunapoweka mitaala yetu tunalenga kwamba wanafunzi wetu lazima wafundishwe au wapitie huku wajue kwamba tunalenga kwenye viwanda hivi.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, pamba sasa hivi bado pamba tunapeleka nchi za nje tuna-create employment kwa wenzetu. Tunanunua mitumba au tunanunua nguo kwa bei mbaya. Baada ya kufanya kazi na hawa wenzetu donors wanapenda tuwe donor depended so much that tusiweze kujitegemea maana once tumeweza kujitegemea hawataweza kupata raw materials waka-create employment kwao. Ndiyo maana wakija wanakuja na watu wao wenye skills. Sisi tunasema ooh wale ambao hatuna mje nao kwa nini sisi hatu-train watu wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nafikiria kama alivyokuwa anasema Mheshimiwa Kimei pale walimu wetu wapelekwe nje wapate exposure, short of that tutakuwa hatufiki mbali. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nichangie katika Wizara hii nyeti ya Kilimo. Labda niombe tu kusema kwamba nilisikia vizuri au nilijisikia vizuri nilivyoona Waziri akisema kwamba hiki kilimo ambacho kinaendeshwa na asilimia 65 ya Watanzania hakina tija. Kwa mantiki hiyo nika-expect kwamba atakuja na mpango mkakati wa kwamba tuwe na commercial farming ya big farmers ambao wataweza ku-supplement kulima kilimo hiki cha wenzetu hao wadogo.

Mheshimiwa Spika, mwisho nikajiuliza kwamba kwakweli sijaweza kuona kama tunasheria ya kulinda ardhi ya kilimo najua tunasheria ya kulinda mazao kahawa, tumbaku lakini sijui kama tuna sheria ambayo inalinda ardhi ya kilimo. Kwanini ninasema hivyo unakuta mara nyingi kumekuwa na hii migogoro ya kuingiliana Wafugaji na Wakulima moja, lakini la pili Serikali ikitaka kujenga mahali inakwenda kufukuza wakulima wanasema tunataka nafasi hii tugeuze tuwe tunajenga aidha Ofisi za Serikali au tujenge shule kiasi kwamba mkulima anajiona kama mtumwa katika nchi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe umeji-establish kwa miaka mingi ile sehemu umeitafuta ukajua kuna maji pake lakini sasa inakuja Serikali inasema itaku-compensate hakuna kukaa ku- negotiate hakuna kuna kwamba unanihamisha unanipeleka wapi? Haiwatafutii hata mahali pa kusema ndio wana settle kwa ajili ya kujenga nyumba zao na kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matokeo yake mashamba ambayo mkulima ameyaboresha kwa muda mrefu anapewa fedha kidogo anaambiwa nenda utatafute sehemu nyingine, swali ni kwamba kule anakoenda kutafuta ana uhakika gani baada ya miaka mitano hatahamishwa tena kwa hiyo, nilikuwa ninaomba nipate hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine sisi najua Tanzania hatuna uzoefu wa kulima kilimo cha umwagiliaji in such commercially sasa ninajiuliza hivi kwanini hatuendi kujifunza kwa wenzetu Kenya, kwanini hatuendi kujifunza kwa wenzetu South Africa! Kwamba ardhi lazima utenge ardhi kubwa kuonesha kwamba hizi hekta labda 100,000 au hekta 200,000 tuna-specialize kwenye mazao say Alizeti. With that tunakuwa forward na backward linkages ambapo utaweza kuweka miundombinu inayotakiwa, miundombinu ya umwagiliaji, miundombinu ya umeme na barabara hapo hapo unaweka kiwanda kitakacho-process tuna vijana wetu wanamaliza SUA tuna vijana wetu wanamaliza vyuo vingi hivi vya Kilimo, hawana ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suppose Serikali ingekuwa imetenga haya maeneo makubwa na hati zipo wakatengeneza infrastructure wakawasaidia hawa vijana wakawapa mikopo ya kama miaka mitano bila kurudisha ili waweze ku-produce hiyo si inge-create ajira ambayo ingehakikisha vijana wetu wanashiriki katika uchumi wa nchi hii.

Mheshimiwa Spika, najua kwamba kuna-documents in come across imeandikwa na Mmarekani mmoja wanasema ‘American needs to keep Africa impoverished ili nchi za Marekani, Ulaya, Asia waendelee ku-survivor. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sasa hivi kilimo chetu kinategemea fedha za umwagiliaji kutoka kwa donners na hivi fedha kwa 90 percent hizi fedha haziji intime.

Mheshimiwa Spika, maana yake zitukwamishe ili tushindwe tuendelee kuwa impoverished kwa hiyo, ningeomba kwamba kama Serikali ipo serious itenge fedha za umwagiliaji nakumbuka mwaka 2019 kulinunuliwa mitambo ya kuchimba mabwawa Mheshimiwa Bashe labda anaweza kukumbuka lakini sijui kama ile mitambo mpaka leo imetumika na kama imetumika imetumika wapi? Kwa hiyo, ina maana nchi yetu tunaweza kuweka mikakati mizuri lakini utekelezaji ukawa mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia nchi zetu za Kiafrika, Afrika nzima ni kubwa inafikia ukubwa ukiunganisha Marekani, China pamoja na Europe lakini leo tunakwenda China kuomba misaada kwa nini, lazima tujiulize kwamba mipango yetu tunayoipanga siyo mizuri na kama Kilimo ndio tunategemea kitutoe basi lazima kipate priority na kiwe well planned ili tujue kwamba kweli tunaweza kutoka katika umaskini huu. Kwa hiyo, ninachoona ni kwamba Wizara zetu hazina mawasiliano. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuhitimisha hoja ya Kamati yangu. Natambua kwamba umenipa dakika tano tu; pamoja na kwamba ningependa ni-respond kwa kila mmoja aliyesema, kwa muda wa dakika tano sitaweza kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitambue tu kwamba waliochangia upande wa hoja za PAC ni Mheshimiwa Bakar Ahmad, Mheshimiwa Aysharose Mattembe, Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mheshimiwa Venant Daudi, Mheshimiwa Aida Khenani, Deus Sanga, Mheshimiwa Samuel Songe na Makamu wangu, Mheshimiwa Japhet Hasunga.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia yale yote ambayo Mheshimiwa Japhet Hasunga ameyasema, ni kama ame- summarize hoja yote, tunataka Serikali ikaifanyie kazi. Kwa kutambua kwamba Serikali imeweza kujibu hayo machechi ambayo waliweza kuyajibu; na kwa kuwa tunajua kwamba sisi PAC hatu-rely kwa majibu ya mdomo, ni mpaka tena CAG aende a-verify hayo mliyosema, napenda kusema kwamba nitambue michango yote ya Waheshimiwa Mawaziri ambayo Kamati tumeipokea. Ni imani yetu kwamba Serikali itatimiza wajibu wake ili sasa katika kaguzi zijazo Kamati ifanye ufuatiliaji wa utekelezaji wa Maazimio ya Bunge.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuchangia hoja ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC).

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, naomba kutoa hoja kwamba sasa Bunge lako likubali maoni na mapendekezo yaliyotolewa na Kamati ili yawe maazimio ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili kuweza kuchangia katika bajeti hii ya Serikali. Pia nitumie nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuniwezesha kufikia siku hii ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nipende kuungana na Wabunge wenzangu hasa akinamama kwa jinsi ambavyo tumeona hizi siku 100 za Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, ambazo zimeonyesha kwamba nyota nzuri huonekana asubuhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, alipotuita pale kwenye mkutano sisi akinamama kwa kweli alizungumza maneno ambayo yalitugusa akinamama wote kwa ujumla na pia Bunge waliona upweke walivyoona akinamama hatupo Bungeni. Kwa hiyo akajua kwamba akinamama ni watu muhimu katika jamii yoyote ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee mambo ya TARURA, kuongeza ile Sh.100 kwenye kila lita ya mafuta ni jambo nzuri, lakini kama fedha hii haitakuwa ring fenced, kama fedha hii haitatumika specifically kwa ajili ya kutengeneza barabara za vijijini na mijini iliyoko under TARURA, dhambi hii haitamwacha salama Waziri Mwigulu Nchemba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua ni wazi kwamba kuongeza Sh.100 kwenye kila lita la mafuta itaongeza gharama za vitu mbalimbali ikiwepo usafiri wa malori ambayo yanabeba bidhaa mbalimbali kupeleka vijijini. Kwa hiyo, kama wananchi hawataona kwamba kweli zile barabara zimetengenezwa, watajua kwamba hapa Serikali ilikuwa inataka kuwatumia kwa kuwadanganya ili na sisi Wabunge tui-support hii measure iliyochukuliwa, halafu sijui hii lawama kama haitafanya kazi ile fedha hiyo iliyotegemewa, Bunge hili tutaficha wapi sura zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nina wazo moja tu au nina weza kutoa maoni kidogo. TARURA wamekuwa hata vijijini wakitumia contractors au wakandarasi. Hawa wakandarasi wanakuja kutengeneza barabara hizi wakati wa kiangazi ambayo kwa kweli tunategemea iwe hivyo, lakini wanachofanya yale ma- grader wanapitisha mara moja, mtu ukipita unaona barabara inatengenezwa, baada ya miezi miwili mvua ikinyesha, barabara hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunaotoka sehemu za milimani tumeona pesa nyingi zimetumika sana kwa TARURA, lakini mifereji haitengenezwi, zile sehemu korofi hazitengenezwi imara, matokeo yake baada ya muda mfupi tu mvua ikinyesha mara moja, mara mbili barabara hazipitiki, mabasi hayaendi, malori hayaendi, balaa kubwa kwa wananchi wakati fedha za mlipakodi zimetumika kwa ujanja, ujanja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nishauri kwamba wakati nafanya internship kule ILO - Geneva nakumbuka kwamba kazi kubwa ambayo ILO alikuwa anasisitiza ni labour intensive, activities hizi zitumie labour zaidi kuliko equipment na kwamba equipment itumike pale ambapo panaonekana kuna hali ngumu ambayo haitaweza kutumia wananchi. Kwa mfano, wakati huko nyuma tulikuwa tunaona kwamba kulikuwa na hizi zinaitwa PWD – Public Works Departments vimewekwa vibanda kila sehemu za barabara zetu na wale wafanyakazi walikuwa wanapewa vifaa kwamba wao wana-monitor, wakiona kuna sehemu ina shida wana-repair mapema.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nashauri, Serikali yetu hii izungumze na TARURA wajiongeze, wafundishe wanavijiji wetu, vijana wetu, kule kwenye vijiji, kwenye kata jinsi ya ku- repair kufanya periodical maintenance ya hizi barabara, wawape vifaa kama machepeo, wheelbarrows, mafyekeo, ambavyo wao baada ya contractor kuondoka wataendelea na ile maintenance ya zile barabara ili ziwe sustainable. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza kutumia ile kama wanavyotumia force account, kuwe na posho ya kuwalipa hawa vijana, kwanza wata-create employment; pili watahakikisha kwamba zile barabara zinapitika throughout the year. Halmashauri zetu kwa mfano halmashauri ya Wilaya ya Same hatuna hata grader, hatuna hata equipment, ukichukua grader la kutoka Moshi kupeleka kwenye vijiji vyetu unaambiwa ulipe kwanza milioni tatu la kuliondolea pale na kila siku unalipa laki tisa. Sasa hapo kwa fedha hizi ambazo naamini ni nyingi, naamini Serikali ikiwa na nia njema itaweza kusaidia Halmashauri zikapata hizi equipment, zikaongeza ma-engineer wa TARURA ambao wataweza ku-monitor hizi activities ambazo zinafanywa na vijana wetu ambao tutaweka hizi building brigades au road brigades. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hilo nataka nizungumzie pia vikundi vya ujasiriamali, ile ten percent inayotengwa kwenye halmashauri. Experience imenionyesha kwamba akinamama licha ya jinsi ambavyo Rais wetu alizungumzia kuhusu hela ndogo inayotolewa kwenye hivi vikundi, lakini once wakishapewa zile fedha mgogoro unaanzia pale, vikundi vinasambaratika, wanagawana zile fedha na kazi haifanyiki ile iliyotarajiwa. Fedha hizi zilikuwa zinatengwa ili ziwe revolving fund, ili ziwe zinarudishwa wengine wanapewa, lakini haionyeshi popote pale kwamba hizi fedha zimekuwa zikirudi na vikundi vingine kupewa fedha hizo hizo imekuwa kila mwaka Serikali inatoa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nashauri kwamba fedha hizi badala ya kutolewa cash, kuna Maafisa Maendeleo ya Jamii, kwa nini wasitumie hizi fedha kununua equipment wakawapa vile vikundi, maana wao ndio wana- mobilize vile vikundi, wakawapa na kuwasimamia kuhakikisha wanafanya ile kazi waliyoitarajia. Kwa hiyo ningeomba kwamba Serikali iliangalie hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka kuzungumzia, napendekeza TRA fedha inayotengewa iwe ya kutosha ili iweze kuajiri wafanyakazi watakaoweza kukusanya kodi. Pia CAG nashauri kwamba apewe hela za kutosha, apewe ruhusa I do know you call it ruhusa ya kuajiri wafanyakazi, because ameongezewa kazi ya ku-audit miradi zaidi kwa ajili ya kuona kwamba fedha za umma zinatumika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka CAG kama alivyosema afanye -real time auditing aweze ku-curb problems za kupotea kwa fedha kabla hazijawa zimetumika vibaya, halafu ndiyo aje kukagua. Kwa hiyo tungesema kwamba CAG akipewa hizi fedha mapema anaweza kufatilia jinsi ambavyo bajeti hii itatumika. Tumeona huko nyuma kwa mfano kuna Mfuko wa Hifadhi ya Wanyamapori ambao ulipata bilioni nne kwa ajili ya kufanyia usanifu wa jingo. Tangu wamefanya usanifu huo ni miaka minane sasa lile jengo halijajengwa ambalo ni la Mfuko wa Hifadhi ya Wanyamapori, bilioni nne zimepotea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna ndege ambayo imetengenezwa zimetumika karibu bilioni nne, lakini hiyo ndege haijawahi kunyanyuka chini, ni mbovu siku zote. Sasa tunachosema ni kwamba, laiti CAG angekuwa na fedha za kutosha akaajiri wafanyakazi wa kutosha, akawa anafanya real time auditing angeweza ku-curb hizi proliferation ya hizi fedha zinazopotea bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri pia nchi yetu iunde think tank la watu wenye busara, wenye hekima wa uchumi, wenye kujua mambo ya uchumi, ambao wanaweza kuishauri Serikali yetu jinsi ya kuweza kufanya ufuatiliaji wa yale ambayo yanawekwa kwenye bajeti na jinsi ambavyo fedha inatumika ili kusudi isiwe tunapanga hiki na kinachofanyika ni kingine. Naamini kwamba hii pia itafanya mambo ya monitoring na evaluation ili tujue kwamba kweli fedha ya umma inatumika jinsi ilivyopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hoja ya Kamati zetu hizi tatu za PIC, LAAC na PAC. Kwanza ninakushukuru sana kwa vile umerudisha heshima ya Bunge hili, umekumbusha Watanzania wote kwamba Bunge hili lina meno na kwamba kweli kipindi hiki hatuna mchezo, kwa hilo unamuunga Mama Samia Suluhu Hassan mkono, kwa vile nakumbuka tulivyokuwa Tanga kwenye semina ya Polisi wakifundishwa mambo ya maadili ambapo CAG alikuwepo alimsifia sana CAG kwa kazi yake kubwa anayoifanya, alikemea sana Polisi wanavyofanya ubadhilifu wa fedha za umma na akakagiza kwamba kwa kweli taarifa za CAG zifanyiwe kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa kutupa muda wote mrefu huu wa kuchanganua ripoti ya CAG tunakushukuru sana, maana tumeweza kuongea na tutaweza kuongea mengi. Ninakuomba kwa muhtasari kidogo kabla sijachangia nieleze Bunge lako Tukufu wajue kwamba kwa mwaka ulioishia Juni 30, 2022 CAG alifanya kaguzi kwa jumla taasisi 331 za Serikali Kuu. Pia kwa upande wa mashirika ya umma alifanya ukaguzi mashirika 200 na pia alifanya ukaguzi wa ufanisi kwa taasisi12, jumla alifanya kaguzi 543. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimewaeleza hilo kwa kuzingatia kwamba Kamati ya PAC kwa nafasi ambazo tunapewa kisheria, tumeweza kupitia chini ya asilimia 10 ya haya mashirika yote, kwa hiyo niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba kwa nini ripoti ya CAG imetawanywa kwa kila mtu? Ni kwamba tupitie, tuangalie, tuhoji, ndiyo kazi ya Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, isionekane ni hii PAC, LAAC au PIC yenye jukumu lile, maana kama ni kupitia kila mahali basi ingebidi iwe kazi ya kila siku kama ambavyo nchi nyingine wanafanya. Mimi ni Makamu Mwenyekiti wa SADCOPAC, PAC’s zilizoko Kusini mwa Afrika, kuna nchi ambazo wao throughout wanafanyakazi ya kupitia kaguzi za PACs zao na kuhakisha kwamba wanamaliza taarifa za CAG na kuhakikisha kwamba wanazimaliza ndipo wazipeleke Bungeni.

Mheshimiwa Spika, kwa taratibu zetu mashirika ni mengi na najua kwamba kwa hilo kwetu itakuwa shida kidogo, labda hapo baadae Bunge lako Tukufu linaeza kutoa muda zaidi tukaweza kupitia mashirika mengi yenye utata.

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa hiyo background niseme tu kwa kifupi kwamba, kwenye ripoti yetu tuliyoitoa kwa ukaguzi uliofanywa na CAG kwa mwaka wa 2019/2020 ripoti yetu tuliyoileta Bungeni hapa mapendekezo yote tuliyoyatoa ambayo Bunge lako Tukufu liliyachukulia kama maazimio mengi hayakufanyiwa kazi, na mengi yamejirudia katika taarifa yetu hii, ndiyo maana unaona kigezo chetu kikubwa tunachoweka ni kupitia yale mashirika ambayo tungeweza kusema au zile taasisi tunazoweza kusema wanashingo ngumu. Bunge lako Tukufu linatoa maagizo hawayafuati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikizungumzia kwa mfano mwaka jana ripoti yetu ya TRA ilikuwepo, TCB, TIB yapo, TANROADS ipo, NFRA ipo, hapa tunayarudia tena.
Mengine hatukuweza kuyapitia kwa sababu gani? Kama ni occurrence imefanyika mara moja ile ina utaratibu wake mwingine lakini zile ambazo zimejirudia tunaona hao watu siyo wasikivu na hawako tayari kufuata maamuzi ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, ukiangalia TRA kwa mwaka huu Juni 2021 wameshindwa kushughulikia madeni ya trilioni 7.5, mwaka jana walishindwa kushughulikia madeni ya Trilioni Tatu. Tuliwapa maagizo kwamba washughulikie madeni hayo, kama wenzangu waliopita walivyosema waliona kwani tusiposhughulikia tutafanywa nini? Hili Bunge si litasema tu halafu basi yanaisha? Ndiyo maana unakuta asilimia 95 katika mwaka mmoja ya kodi zile madai hayakufanyiwa kazi. Sasa swali tunalojiuliza hivi Serikali yetu itapata wapi pesa za maendeleo kama tunadai fedha Trilioni Saba kwa mwaka huu tunaozungumza? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia mapungufu katika mfumo wa i-tax (Income Tax Management System), Bilioni 11 hazikuweza kuwa captured. Na unaambiwa mfumo una matatizo na hili tulishawambia hata ripoti iliyopita kwamba, huu mfumo unatengenezwa na binadamu kaushughulikieni msipoteze kodi zetu. Wamekuwa na shingo ngumu leo tena tunayaona haya haya. Kwa hiyo ninachosema ni kwamba umeturudishia heshima yetu na nimesikiliza Wabunge wote wakiongea na kuonesha jinsi ambavyo kipindi hiki hakuna msalia mtume. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, TANROADS, kwenye Bohari, dawa zinaharibika, wazee hawapati dawa wakienda dispensaries, wanaambiwa hakuna. Tumeona yaliyofanyika kwenye fake VISA huko. Tumeona ujenzi wa vihenge ambaye anapewa Mkandarasi wa nje kana kwamba sisi hatuwezi kujenga vihenge na ameondoka na hakuna anachofanyiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo ukianagalia kumekuwa ni kwamba kumekuwa na dharau kubwa sana kwa upande wa wale wenzetu ambao walipewa jukumu la kugawa au kutengeneza miradi mbalimbali kwa manufaa ya nchi hii. Kwa hiyo, tuseme hivi kama wakati ule aliposema Hayati Baba wa Taifa kwamba sababu tunayo, Bunge hili tuna sababu ya kuwawajibisha hao watu nia tunayo na uwezo tunao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukuombe kama itakupendeza italetwa labda kwenye mapendekezo, tuna Kamati yetu ya Maadili, yale yote ambayo Waheshimiwa Wabunge ambayo wanayasema, nafikiri itakuwa wakati muafaka. Waitwe hawa hawa watu kwenye maadili wajue Bunge lina meno ili Bunge lako tukufu liweze kupewa ripoti kamili ya jinsi ambavyo ubadhilifu huu mkubwa wa fedha za umma umefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mungu kwamba mimi nipo kwenye Kamati ile na Makamu wangu Mheshimiwa Hasunga pia yupo kamati ile. Kwa hiyo, tutatoa yote, maana tumepitia ripoti yote ya CAG ni kwamba hatukuweza kuifanyia kazi yote, lakini wote tumeisoma na tunajua madhaifu yaliyofanyika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikuombe, mengi yameshazungumzwa na kazi yetu kubwa ni kwamba tutajua tulete mapendekezo gani katika Bunge lako Tukufu ili yachukuliwa hatua. Nisisitize kwamba, Mama Samia Suluhu Hassan, ambaye wakati wa Hayati Rais Magufuli, alikuwa halali anaamshwa usiku wafanye kazi; leo anakuwa Rais anafanya kazi, watu wachache wanchukua hela wanatia mfukoni halafu wanajua Bunge litatufanya nini. Uzuri Rais mwana mama, Spika mwana mama, Wenyeviti wa Kamati ya PAC na LAAC wana mama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatukosei, kama tumeweza kuwafundisha wanaume kuvaa suruali, tumevalisha nepi, tumewanyonyesha, tukawalea, leo tunashindwa kuwawajibisha. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia Hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023. Mimi nitajikita zaidi katika ule ukurasa wa 32 wa hotuba hii ambayo imezungumzia juu ya wafugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, utakumbuka kwamba jambo hili tatizo kubwa la wafugaji na wakulima limekuwa ni janga la Taifa. Watu wameuana kwa ajili ya mipaka, wafugaji wakienda kulisha kwenye mashamba ya wakulima, sasa mimi naomba kwa vile Waziri Mkuu yupo hapa akihitimisha hotuba yake alitueleze hii Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi, kazi yake kubwa ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua wazi kwamba nchi yetu ni kubwa sana yenye square kilometers 947,303 ukiondoa 61,500 unabaki na 885 ambayo ndiyo ukubwa wa ardhi yetu. Kwa sehemu ya kilimo amesema kwamba ni hekta milioni 44 ambazo zinafaa kwa kilimo, ingawa mpaka sasa hizi ni hekta 14.5 Milioni ambazo zinatumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia yote haya ni kwamba nchi yetu haitilii umuhimu wa wafugaji, wanaona wafugaji ni watu tu wa kuswaga ng’ombe na kukimbia huku na huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utakumbuka kwamba nchi yetu inaringa kwamba ni nchi ya tatu katika Afrika kwa kuwa na mifugo mingi Milioni 25, lakini hotuba ya Waziri Mkuu inaonyesha kwamba katika hizo ng’ombe Milioni 25 pato letu limekuwa ni Dola za Marekani Milioni 22,400. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikilinganishwa na wenzetu wa Kenya ambao wao wameweka msisitizo kwenye kufuga kisasa, zero grazing. Utakuta kwamba wao pato lao ni karibia Bilioni Moja za Marekani, wakati ng’ombe wao wanaofuga ni Milioni 21 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Milioni 25 ya ng’ombe wetu wa Tanzania asilimia 98 ni wa kienyeji na wanafugwa kienyeji. Ukiangalia nchi ya Denmark ambayo ina ng’ombe 1,500,000 wao wamepata Milioni 330 USD kutokana na mauzo ya ng’ombe. Kwa hiyo, tunachojiuliza ni kwamba hivi Tanzania tutangoja lini wananchi wetu waendelee kuuana, wafugaji na wakulima kwa ajili ya ardhi, wakati tuna ardhi kubwa lakini haijapangiliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia unakuta kwamba takwimu zinaonyesha eneo la kulima ni kiasi gani, lakini takwimu hazionyeshi eneo la wafugaji ni kiasi gani. Swali ninalojiuliza ni kwamba hawa wataalam wetu wa ugani wa mifugo wao hawajui faida ya zero grazing wala hawajui faida ya cross breeding kiasi kwamba ng’ombe wetu wote ni wa kienyeji ni kiasi kwamba tuna ng’ombe lakini wasio na tija? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninashauri kwamba Serikali yetu kwa vile imeunda Wizara nzima ya Mifugo, Wizara hii ije na mpango mkakati mzima wa kutuonyesha kwamba imetengwa ardhi kiasi gani ya wafugaji na wafugaji hawa wangapi wameshapewa maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Wawekezaji wameweza kutengewa nafikiri Milioni 200 hectors, kwa nini wafugaji wetu wasitengewe maeneo ya kulima? Ni kwamba tunaamini kwa watu wa nje kuliko watu wetu wenyewe, hata fedha hizi ambazo Waziri Mkuu ameweka hapa kuonyesha kwamba ndiyo zimepatikana, naamini sehemu kubwa ni wafugaji wenyewe waliohangaika kuingiza pato hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali mara nyingi wanasema wafugaji wapunguze ng’ombe, lakini hawajaweka kiwango kwamba wapunguze kutoka kiasi gani ifikie kiasi gani, na wakipunguza wanawasaidia nini katika malisho yao na maji yao. Maana wafugaji wanafugaji wanafuga ng’ombe wengi wakijua kwamba hata nusu wakifa watabaki na nunu. Sasa Serikali unapoendelea kusema punguzeni mifugo bila kuweka idadi hujawasaidia wafugaji wala wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine hebu tuangalie hizi Ranchi zetu utakuta kwamba ukienda kama kwenye Ranchi ya Kongwa ina eneo kubwa sana ambalo limetengewa kufuga lakini productivity ya pale haiendani na eneo lile. Hawa ni watu wamewekwa pale wanalipwa mshahara, lakini production ni ndogo mno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba kwa nini Serikali isiangalie haya maeneo nakuona kwamba kama hawa wanaoendesha hizi Ranchi hawawezi kwa nini wasiwape wafugaji wakafanya kazi hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali imeweza kuhamisha wafugaji kutoka Ngorongoro kwenda Handeni, kitu gani kinashindikana kuhamisha wafugaji wale wenye ng’ombe wengi na kuwapeleka kwenye maeneo ambayo wametengenezewa kwa ajili ya ufugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa wenzetu wa huko Kenya tunasema kwamba wanaofuga ni wale ma-settlers lakini what does it mean, settlers ina maana wamefanya zero grazing na wanaweka miundombinu yote inayotakiwa, sisi tunashindwaje ku-settle wafugaji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokiona ni hapa kwamba Serikali ipo tayari kupeleka hela nyingi kwenye migodi tubaki na mashimo baada ya miaka 100 ijayo, kuliko kusaidia wafugaji wetu na kuwaweka mahali, wakawatengenezea biogas, wakawapandia majani, wakawasaidia ile slung ya biogas wakapandia kama mbolea ikasaidia katika kukuza majani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali mna kazi kubwa ya kufanya, hamjatu-impress kwenye upande wa wafugaji. Kwa ajili hiyo, hatuna haja ya kuringa kwamba tuna ng’ombe wengi maana wale ng’ombe wote wamechoka na wachungaji wamechoka hawana tija. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshiniwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii yakuchangia katika mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kuishukuru Serikali kwa kuweza kuajiri watumishi wa TRA. Kamati yangu imekuwa ikipigia kelele sana ufanisi wa kazi wa TRA na tuliona kwenye ripoti yetu tuliyoleta, jinsi ambavyo kumekuwa na shida katika kukusanya kodi. Kwa hiyo, unakuta kwamba madai yanaongezeka kutoka trilioni 3.9 mpaka trilioni 7.5 ambayo ilikuwa kama asilimia 95 ya madeni ambayo hayakukusanywa kwa mwaka wa 2020/2021. Najua kwamba Taifa letu linategemea sana kodi na kama hazikukusanywa na hata hii Mipango tunayoongelea haiwezi kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mimi nataka nichangie tu katika eneo moja, hili eneo liko chini ya sura ya tatu ya maeneo ya kipaumbele kwa mwaka 2023, Namba 332, ambayo inazungumzia kilimo, mifugo na uvuvi, Ukurasa 124. Ni aibu kwa Taifa letu, na ninamuona Waziri Ndaki ananiangalia sana, kwamba, sasahivi Taifa letu hapa tulipofikia na baada ya kuwa na Wizara nzima ya Mifugo bado watu wafugaji, hatuwaiti wafugaji, wachungaji, wanakimbizana na ng’ombe, ng’ombe waliochoka, ng’ombe waliokondeana, halafu ng’ombe hawa wanaenda kulishwa kwenye mashamba ya wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema sisi kazi yetu kubwa hapa kwenye Bunge ni kutetea wanyonge. Hakuna watu wanyonge waliozidi wafugaji na wakulima. Sasa unashangaa tunaacha haya makundi mawili yanamalizana. Hivi karibuni tumeshuhudia watu wakikatwa mapanga, watu wakiuana kwa vile makundi ya ng’ombe yanaswagwa kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine na yanashambulia mashamba ya wakulima. Swali langu najiuliza, hivi tuliunda Wizara nzima ili nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifanya cost benefit analysis ya Wizara nzima na kazi inayofanyika sijui kama ita-balance. Mimi nilitegemea, kama kilimo walivyosema, kwamba wanatenga blocks kubwa vivyo hivyo nilitegemea mifugo yetu, wale wafugaji wetu watengewe maeneo. Wale wenye ng’ombe wengi wanaweza kuelezwa wakaambiwa kwamba tunakupa eneo hili kama linakuwa fenced, kama wanapeleka miundombinu na wao wachangie ili waweze kufuga mifugo ya kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kwamba, Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Kikwete, alilizungumzia sana hili suala la wachungaji akiwa Rais. Aliomba sana Serikali iangalie namna ya kuondokana na kuswaga ng’ombe tuwe wafugaji badala ya wachungaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu Rais Mstaafu Jakaya Kikwete ametoka imekuja awamu ya tano na sasa ya sita. Leo ndio tunaona vita vikubwa sana kati ya wakulima na wafugaji halafu Serikali tunaangalia. Unashangaa hivi hawa wafugaji wana nguvu gani kuliko Serikali kiasi mtu anaamua kuswaga ng’ombe na kuingiza kwenye mashamba ya wakulima? Kwa hiyo umasikini wetu huu tunauzungusha wenyewe, vicious circle ya umasikini wetu wa nchi, matokeo yake tutaanza tena kuomba chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mifugo tunajua faida yake kubwa. Kwanza wenzetu wengi walioendelea wageni wanaokuja nchi hii wana-import nyama kutoka Botswana au kutoka nchi zao, nyama yetu ukila hap ani plastic ng’ombe wale walivyo. Sasa tunashindwaje kuweka viwanda kule Shinyanga tukasaidia watu wetu wafugaji kule wakatengewa maeneo, wakafundishwa kuweka majani ya kisasa, wakatengeneza hata bio gas ili wawe na nyumba zile wasiingie hasara za kutumia umeme huu wa grid wakawa na silage ile ambayo wanaweza wakitoa biogas wanaweka kwenye majani, wanaweka kwenye mimea? Ni kazi ngumu gani kuona kwamba, kule tungeweza kuweka viwanda vya ngozi, viwanda vya maziwa na by products nyingine? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu kwato zile zinatengenezea jelly, ile gundi. Sasa sisi Tanzania tunacheza. Angalia wenzetu wa Botswana wameona kwamba sasahivi almasi walikuwa wanaitegemea, Ulaya na Marekani sasahivi wanatengeneza almasi fake, hawana soko, wamezamia kwenye mifugo tu. Na Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Mchemba ametuwekea data jinsi ambavyo wenzetu uchumi umekua katika muda huu mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana na Waziri wangu wa mifugo namheshimu sana, Waziri Ndaki, hebu angalia tuweke blocks tuchukue vijana wetu hawa waliosomea mambo ya mifugo tuwawezeshe. Hizi fedha zote zinazotolewa kwenye vikundi wapewe, wawezeshwe, watengenezewe maeneo waweze kufuga kisasa. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuhitimisha hoja yetu ya PAC. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuchangia hoja ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na kutambua maelezo ya Serikali kuhusu hoja mbalimbali za Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya Waheshimiwa Wabunge waliochangia ni saba na maeneo waliyowekea msisitizo na Wajumbe ni kama ifuatavyo: -

(a) Kukosekana kwa thamani ya fedha (value for money) katika baadhi ya miradi ya maendeleo;

(b) Upotevu wa fedha za umma zinazolipwa katika riba kwa wakandarasi;

(c) Ukiukwaji wa Sheria ya manunuzi na kanuni zake na kanuni zake katika utekelezaji wa baadhi ya miradi;

(d) Kuongezeka kwa gharama za utekelezaji katika baadhi ya miradi, (variations).

(e) Kutofanyika kwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kabla ya kutekeleza kwa baadhi ya miradi;

(f) Kukosekana kwa master plan katika utekelezaji wa miradi ya maji nchini na dosari katika usimamizi wa mikataba;

(g) Uwepo wa mwingiliano wa majukumu baina ya taasisi ya Serikali kama vile TAA na TANROADS.

(h) Mifuko ya uwezeshaji wananchi kiuchumi kutofikia malengo ya uwanzishwaji wake kutokana na fedha kupelekwa kwa watu ambao sio walengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati inaendelea kusisitiza Serikali kutekeleza kikamilifu mapendekezo yote ya CAG na Kamati. Aidha, katika kipindi cha kila robo mwaka sekta husika zilizokaguliwa ziwasilishe kwa CAG taarifa ya utekelezaji wa mapendekezo ya ukaguzi ambapo itafanyiwa uhakiki na kisha kuwasilishwa Bungeni kupitia kwenye Kamati kwa ajili ya ufuatiliaji na tathmini ya mwendelezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yetu sisi Kamati kwamba Serikali itatimiza wajibu wake ili kuongeza uwajibikaji katika fedha za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijahitimisha hoja yangu. Nieleze kutoridhika na majibu ya Waziri wa Fedha aliyoyatoa. Kwa kweli mifano aliyoitoa inanipa wasiwasi na nafikiri inaipa wasiwasi na Bunge hili kwamba Serikali itakuwa tayari kusimamia fedha za umma inavyotakiwa. Hakuna justification; upeleke fedha nyingi kwenye miradi ambayo huwezi kui-monitor na ambayo huwezi kujua kwamba certificate hii inatakiwa ilipwe kipindi hiki, kwa hiyo, lazima ilipwe kwa wakati. Uko tayari fedha za mikopo upeleke fedha nyingi na riba ziwe kubwa kuliko hata mradi wenyewe. Hiyo, nafikiri Bunge halitakubaliana na maelezo ya Mheshimiwa Waziri wa fedha. Tunaomba aende akasimamie kikamilifu ulipaji wa hizi certificate. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii kusema fedha zimepelekwa nyingi, na mifano ya kwamba tutajazana wote tukiambiwa tutoke kwenye mlango huo, hakuna fedha ya Serikali inaweza kutolewa kwa emergence namna hiyo, kwamba iende tu, halafu isiangaliwe itatumikaje; halafu izuie kwamba zile certificate ambazo zimefikia wakati wake zisilipwe kwa wakati maana kuna hela nyingi bado zinashughulikiwa huku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri kwa mawazo hayo, nina wasi wasi sana kwamba hata hizi fedha ambazo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anazozileta, kama mtazamo ndiyo huo, hatuna imani kwamba kweli fedha hizo zitatutumika kwa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, licha tu ya kulipa riba kubwa ambayo mkiangalia ni mabilioni ya fedha, matrilioni ya fedha, bado miradi ile haitekelezwi kwa wakati. Sasa kama haitekelezwi kwa wakati tunafanya nini? Ina maana fedha ya mlipa kodi, fedha ya mkulima huyu tulikuwa tunamsemea hapa, ambapo hata kule kwetu kwenye Jimbo la Same Mashariki, Tangawizi iliyokuwa inauzwa kilo shilingi 1,000, au shilingi 2,000, sasa hivi inauzwa kilo shilingi 400 kutokana na changamoto mbalimbali. Sasa uniambie kwamba walipa kodi hao wanaohangaika, wananchi fedha zinaletwa za mikopo nyingi, halafu uambiwe kwa vile zimepelekwa nyingi lazima ucheleshwaji utatokea! Hakuna kitu kama hicho!

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hela ni nyingi lazima iwe na mpangilio, ina maana gani ukakope hela nyingi ambayo hakutakuwa na uwajibikaji? naomba nitahadharishe hilo, nimshukuru sana Mheshimiwa Simbachawene kwa maelezo yake ambayo yametia moyo kidogo, kwamba kwa kweli Serikali itasimamia hayo yote, na tunasema kwamba kunapokuwa na exit meetings za CAG hatuwezi kukaa tena hapa tukaambiwa longolongo zile kwamba hapa ilikuwa hivi hapa ilikuwa hivi, hapa siyo mahali pa ku-justify uzembe ni mahali pa kuwajibisha watendaji wazembe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, Mheshimiwa Simbachawene nimefurahishwa na majibu yako ya kuonesha ukomavu na kuonesha kwamba kweli utasimamia Serikali ipasavyo kuhakikisha kwamba inatumia fedha za umma vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja kwamba sasa Bunge hili likubali maoni na mapendekezo yaliyotolewa na Kamati yetu hii ya PAC yawe maazimio ya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Kilimo. Baada ya Mheshimiwa Halima kuongea, sauti yangu itaonekana imepwaya sana, lakini mnisikilize tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nami niungane na Wabunge wenzangu kwa kumpongeza Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo ameifanya ya kuipaisha nchi yetu mpaka sasa hivi hata Kimataifa tunajulikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, maana najua nina muda mfupi sana, nimwambie tu Waziri Bashe, kweli tunapenda mambo ya block farming, lakini isiwe to the expense ya wakulima wadogo. That is one. But two, tujue kwamba block farming inahitaji umwagiliaji sana, na umwagiliaji huo uwe wa drip au wa system gani, ambao hautaleta siltation. Tuangalie basi tume yetu ya umwagiliji kama ina capacity hiyo ya kuchukua hii role ya kufanya hii block farming na hii programme ya BBT kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia ripoti ya CAG ya ukaguzi wa kiufundi, 2018/2019 mpaka Januari 2019/2020 – 2022/2023, inaonesha upungufu mwingi ambao uko kwenye tume yetu hii ya umwagiliaji. Nitasema machache tu ambayo ni key kwa ajili ya argument yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, tume hii haifanyi upembuzi yakinifu kabla ya kuanza ujenzi wa miradi ya umwagiliaji. Hii tunaweza kusema kwamba tangu mradi ukianza umeshakufa kabla hata haujasimama. Pili, kuna udhaifu mkubwa kwenye kuzingatia Sheria ya Manunuzi. Maana yake ni nini? Fedha ya umma itatumika vibaya sana kama Sheria ya Manunuzi haifuatwi. Tatu, hii Tume ya Umwagiliaji haifanyi uhakiki wa viwango vya ubora wa miradi, na hivyo miradi mingi imeonekana ina kasoro sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu kuna miradi ambayo imekuwa ikichelewa sana kukabidhiwa, na hivyo inaongeza gharama katika kuendelea kutekeleza. Haya yote yanafanya tujiulize, hivi tunapoenda kwenye kufanya block farming na kama tume yenyewe ndiyo hii hii, na jinsi inavyo-operate ni hivi hivi, kweli tunategemea mafanikio? Kama Mheshimiwa Halima alivyosema, kwamba hizi fedha nyingi ambazo zinaenda kwenye miradi hii ambayo tunaona kuna upungufu sana katika hii tume ambayo ndiyo tunaitegemea, zingekwenda kusaidia wakulima wadogo wenye skimu zao kutengeneza vizuri, nafikiri tungefanya mazuri zaidi, maana naona hatujajipanga vizuri kuhusu block farming. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, linalonisikitisha kubwa zaidi, tukiangalia pia upungufu huo, kwenye bajeti ya Tume ya Umwagiliaji kwa mwaka wa fedha 2022/2023 iliidhinishwa shilingi bilioni 257.5 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya umwagiliaji, lakini hadi kufikia Februari, 2023 ilikuwa imetolewa asilimia 18 tu ya fedha iliyotakiwa, yaani katika miezi minane ni shilingi bilioni 46.68 tu zilizokuwa zimetolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiingii akilini kwamba katika kipindi hiki cha robo mwaka kilichokuwa kimebaki, tume itaweza kutumia shilingi bilioni 210 wakati kwa miezi minane ilitumia tu shilingi bilioni 47. Kama hivyo ndivyo, hata huu mradi wa block farming nina mashaka sana kama utafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kwamba kweli wakulima wadogo wanahitaji kusadiwa sana, ukichukulia mfano kama alivyosema Mbunge wa Same Mashariki. Kule kwetu miradi mingi ya mpunga ambayo ilisaidia sana kulisha Mkoa Tanga, Kilimanjaro na Arusha ilikuwa ni ya kilimo cha umwagiliaji. Ukiangalia kilimo cha umwagiliaji cha skimu ya Ndungu, mfereji wa fidia, Kalinga Maore na hizo za Kihurio zilizosemwa zote zilikuwa zinalisha mikoa hiyo mitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu miradi hii imejengwa tangu mwaka 1999 imetelekezwa. Kwa mfano, mradi wa fidia wa Ndungu, sasa hivi mvua ikinyesha kubwa inakuwa ni shida kwa wakulima hao. Mradi uliojengwa kwa msaada wa kutoka Japani ambao hatukuweza hata kuuhudumia, leo mvua ikija ni mafuriko kwa kwenda mbele, mashamba yanaharibika, zile barabara zilizotengenezwa za kuingia mashambani zinaharibika. Matokeo yake, badala ya kuwa baraka, mvua inakuwa laana kwa wakulima wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameomba wafanyiwe kitu kinaitwa kudebua mifereji ile. Nilishangaa kwamba kweli tume ilipeleka mitambo ile ya kudebua, lakini bila tume kuwasiliana na Halmashauri, ikitegemea Halmashauri itatoa Shilingi milioni 80 ikapeleka mashine ile, equipments zile, zikakaa mwezi mmoja na kitu bila kufanya kazi yoyote. Mwisho zikaondolewa. Kwa hiyo, ukiangalia usimamizi wa vyombo vyetu ni hafifu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiingii akilini kwamba unawezaje kutoa mitambo Dodoma uipeleke Ndungu ikae mwezi mzima na zaidi, machine iko pale yame ku tide up, wafanyakazi wako pale hawalipwi au watalipwa na hela ya Serikali, lakini kazi haifanyiki. Maana Shilingi milioni 80 Halmashauri haijatoa. Sasa hapo tunajiuliza, hivi kweli are we serious? Are we serious kwamba tunataka kulima kilimo kikubwa, lakini cha hawa wadogo ambao miaka yote hii ndiyo wametubeba, tumeshindwa kukilima!

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia shirika letu la NFRA haliweki akiba ya mpunga au maharage au mbegu za alizeti, at most inaweka tu mahindi na nafaka nyingine inaitwa mtama. Sasa ukiangalia wananchi wengi wanakula wali, halafu NFRA haiweki hiyo kama akiba. Pamoja na upungufu uliyooneshwa jana, juu ya kwamba NFRA inakuwa na akiba ya kama siku tatu na nusu, hata huo mpunga haupo kwenye list. Sasa unajiuliza, hivi nchi yetu tunakwenda wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri kwamba Mheshimiwa Waziri hebu u-rethink kwamba hivi hii BBT kweli itafanikiwa kwa approach hii tunayokwendanayo? Tuko too theoretical in the sense that BBT au block farming inahitaji a lot of mechanization. Sasa hivi ukimchukua tu kijana uliyemchukua mtaani umfundishe miezi minne halafu umpe kazi kubwa kama hii I don’t think kama tutafanikiwa. I wish tungechukua mashamba karibu na wenyeji wenyewe tukawa-identify wale vijana ambapo maeneo yale wanajihusisha na kilimo, wakapewa hiyo kazi, wakafundishwa, because at least wana A, B, C ya kilimo na itakuwa kwenye Mkoa ule au Wilaya ile. Kwa hiyo, hata kijana aki-abscond, wapo watakaoendeleza. Sasa tunawatoa Mikoa mingine, tunawapeleka mikoa mingine. Kesho hali yake ya kifedha imekuwa nzuri, anaamua kuacha lile shamba, unamfanya nini? Unamfanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, yangu ni hayo machache kwamba hebu tu-rethink approach ya hii block farming kwamba tumejiandaa vipi? Kwa gharama hizi zilizotajwa, kwa kweli sidhani kama ni sustainable, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya ujenzi na uchukuzi. Niseme kweli kwamba, Wizara hii kweli ni kubwa sana na inajitahidi sana kufanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaenda straight kwenye shirika letu la ATCL. Kitendo cha kusema tunafufua shirika hili na kununua ndege nyingi kilikuwa ni kitendo kizuri sana. Kwa hiyo, niseme kwamba, Serikali haikufanya makosa kuamua kufanya hivyo. Niseme Shirika hili la ATCL limejitahidi sana kufanya kazi pamoja na kwamba, limefanya katika mazingira magumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kwamba, Mheshimiwa Profesa Mbarawa amejitahidi sana kuona shirika hili linasimama, lakini jambo moja ambalo linanifanya nione kwamba, kwa nini hiki kitendo cha kuweka ndege hizi kwenye Shirika la Ndege hili, TGFA kwamba, ndio limiliki ndege zile kwa nia ya kwamba, ndege hizi zisingekamatwa kutokana na madeni ya Serikali, lakini imeshaonekana kwamba, hili halipo. Kama halipo kwa nini ndege hizi hazirudishwi au hazipelekwi ATCL? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mkataba huu wa ndege wa ATCL pamoja na TGF umekuwa ukileta madeni makubwa sana kwa shirika hili na kufanya shirika hili lionekane kwamba, linaweza lisiwe na mwendelezo, yaani tuseme questionable going concern. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba, urari hasi wa kiasi cha shilingi bilioni 157.7 kwa ATCL umeletwa na ukodishaji huo. Kwanza tuangalie Ripoti ya CAG katika mwaka 2021/2022 ilionesha kwamba, ATCL ilitumia shilingi bilioni 29.4 kwa matengenezo ya ndege zake, lakini hapohapo ilitakiwa pia ipeleke shilingi bilioni 25.38 kwenye TGFA kama gharama za matengenezo licha ya kwamba, bado kuna zile gharama za ukodishaji ambazo ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika speech ya Waziri, ukurasa wa 267 umesema kwamba, ATCL imeweka mikakati mizuri ya kuweza kupunguza gharama za uendeshaji. Kinachonishangaza ni kwamba, Mheshimiwa Waziri hakutaja hili tatizo la TGFA kuwa bado ndio wamiliki wa ndege hizi ambazo zinafanya kunakuwa na double cost ambazo kwa njia yoyote ile hatuwezi kupunguza deni hili au madeni haya ya Air Tanzania. Commitment iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Ikulu mwaka 2021 alisema kwamba, ifikapo tarehe 30/06/2022 umiliki wa ndege za ATCL utakuwa chini ya ATCL yenyewe kutoka TGFA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa ukiangalia tangu ahadi hii ilipotolewa kwamba, umiliki huu ungehamishwa, mpaka leo ni karibu mwaka mzima na hamna kilichofanyika. Kufuatia malimbikizo ya kukodisha ndege hizo toka TGFA takribani shilingi bilioni 113.5 na deni la Mfuko wa Matengenezo ya Ndege takribani shilingi bilioni 60, haya ni madeni makubwa sana ambayo yatafanya shirika hili lishindwe kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nieleze tu kwa kifupi kwamba, nini athari kubwa ambayo athari zake zitaletwa na huu uhusiano kati ya TGFA na ATCL. Ni kwamba, ATCL inaweza kufutiwa uanachama wake katika Shirika la Mashirika ya Ndege Duniani (IATA). ATCL inaweza kufutiwa mifumo ya kimataifa ya ufuatiliaji wa mizigo. ATCL inaweza kutolewa katika mfumo wa usuluhishi wa mauzo ya tiketi duniani (IATA Clearing House). Shirika hili linaweza kutolewa katika mfumo wa uuzaji na usambazaji wa tiketi duniani (Global Distribution System), pia ATCL inaweza kushindwa kupata vibali vya kufanya safari katika Mataifa mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia pamoja na mikakati kwamba, ATCL inataka ifanye interlining and code sharing, lakini kwa urari huu ambao ni hasi hili linatia mashaka sana na ukiangalia kwamba, ATCL haiwezi kukopesheka kutokana na hali halisi ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa ushauri ufuatao, kwamba, Serikali ifute malimbikizo yote ambayo yamepelekwa katika shirika hili ambayo ni takribani bilioni 113.5 na deni la Mfuko wa Matengenezo ya Ndege ambalo ni takribani shilingi bilioni 6.0 na kwamba, umiliki huu wa ndege upelekwe moja kwa moja kwa ATCL badala ya kuwa TGFA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, faida gani tunatarajia kwamba, ATCL ikiwa mmiliki moja kwa moja? Ni kwamba, ndege zote za ATCL kama zile Air Bus, Boeing 77, 787A.8, Dreamliner, kwenda vituo vilivyopangwa kama Johannesburg, London, Nigeria na sehemu nyingine, hivyo kufanya ndege hizo kuweza kufanya kazi zake kikamilifu. CAG ameonesha kwamba, ndege hizi kwa kutokufanya kazi zake kikamilifu kwenye full capacity zimeleta hasara ya shilingi bilioni 45 katika mwaka 2021. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni wazi Waziri hili analiona na ndio maana amekwepa kuweka taarifa hii ya ubia kati ya ndege hizi kwa TGFA. Kwa hiyo, anajua kwamba, tumelisema sana kwenye Kamati yetu ya PAC, lakini hakujachukuliwa hatua yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, faida gani itapata ATCL pia, kwa kuipa umiliki wa ndege zote? Ina maana kwamba, gharama zake za uendeshaji zitashuka kwa asilimia 30 na hasara kuondolewa kwa asilimia 171 ili ndege hizo ziweze kuonekana kwamba, kweli zina-perform vizuri. Kama ATCL itaweza kumiliki ndege zake zote itaweza kuanzisha auxiliary services zake ambazo ndio zinaleta faida kubwa katika mashirika ya ndege. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri Profesa Mbarawa akija kuhitimisha hotuba yake alieleze Bunge lako Tukufu kwa nini imechukua muda mrefu hivi TGFA kukabidhi ndege hizi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kunaundwa Kamati, tunajiuliza, hivi wakati ndege hizi zikiamuliwa kupelekwa TGFA Kamati ilichukua zaidi ya miaka miwili kuzungumza suala hili? Kwa ajili hiyo, niombe kwamba, Serikali ione athari hizi na ielewe kwamba, hili shirika pamoja na kwamba, tumeweka mikakati mingi, inatumia fedha nyingi za Serikali ambazo ni fedha za umma, lakini bado tumelifunga miguu na mikono halafu tunaliambia likimbie. (Makofi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali iweze kuweka wazi kwamba, kweli itatoa lini, iwe na commitment ambayo ile ya Katibu Mkuu huyu wa Ikulu ambaye sasa hivi ndiye Katibu Mkuu Kiongozi imeshindikana, mwaka mzima sasa hivi lakini hata hotuba ya Waziri haikuzungumzia suala hili. Kwa hiyo, inasikitisha kwamba, Serikali imechukua muda mrefu sana kuona kwamba, ATCL inatakiwa ifanye kazi, iwe competitive sawa na mashirika mengine duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufikia hapo, nasema kwamba, hayo ndio yangu kwa leo. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika mwaka wa fedha huu 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nipongeze Wizara hii kwa hotuba nzuri ambayo naamini kwamba kama ikitekelezwa kikamilifu italeta matunda chanya. Lakini pia niseme kwamba, kama wenzangu waliotangulia walivyosema, kuwapongeza Spika wetu, Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, pamoja na Mheshimiwa Balozi Liberata Mulamula, kwa kupatiwa nafasi na Serikali yetu kugombea nafasi hizi za IPU na kuwa Katibu Mkuu katika Jumuiya ya Madola. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme hivi; nafasi hizi ni very competitive, watu wanao-compete ni wengi sana, tusije tukafurahi kwamba tumepeleka majina kwa hiyo automatically watapata. Mimi nafikiri ni vyema Serikali yetu ikajipanga vizuri, hasa ikiongozwa na Wizara yetu hii ya Mambo ya Nje kuhakikisha tunafanya kampeni ya kufa mtu ili nafasi hizi tuzipate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi za Afrika Magharibi zimeweka watu wao kwenye nafasi hizi za kimataifa kiasi kwamba wame-benefit a lot kutokana na kwamba wale wafanyakazi wao wanarudisha nini nyumbani. Kwa hiyo ninaomba sana Serikali tusilichukulie lelemama bali tuweke nguvu tukiona kwamba tumekuwa na Katibu Mkuu katika Jumuiya ya Madola, nafasi hii itatupa nafasi kubwa sana katika nchi yetu ya Tanzania kupata mambo mengi, maana mimi nilishapata experience kidogo, nimefanya kazi kidogo kule, kwa hiyo najua kuna nafasi gani kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nizungumzie hotuba ya Mheshimiwa Waziri wetu aliyoileta kuhusu kwamba yeye anaweka mkazo katika diplomasia ya kiuchumi. Tukumbuke kwamba Hayati Benjamin Mkapa hii ndiyo ilikuwa area yake ya kipaumbele miaka 28 iliyopita. Miaka 28 iliyopita aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tatu alisema diplomasia ya kiuchumi ndiyo itakayoongoza Taifa letu katika kutuletea maendeleo ya haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ni miaka 28, hebu tujiulize, katika miaka 28 hii inaendana na yale ambayo tumeyafanya tangu wakati ule mpaka leo? Ni wazi kwamba tuko nyuma sana katika diplomasia ya kiuchumi. Tukiangalia yale ambayo yamefanyika kwa kipindi hicho mpaka leo, hakika utajua kwamba tuko nyuma sana kwa yale yaliyotakiwa yafanyike hadi leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwamba ameunda tume ya kuangalia utendaji wa Wizara hii ya Mambo ya Nje. Ina maana kwamba kuna mapungufu makubwa ameyaona katika Wizara hii. Na hii pia inanipa picha kwamba kumekuwa na mapungufu makubwa. Nikiangalia kwamba katika kipindi hiki cha miaka mitano hii ya mwisho, maafisa masuuli wamebadilishwa badilishwa sana, takriban kila mwaka unapata Katibu Mkuu mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inaashiria kwamba kuna tatizo kubwa mahali; ama wale wanaomshauri Rais, kwamba huyu anafaa kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje, au yale yaliyotegemewa siyo wanayoyafanya. Kwa hiyo hapo tuliangalie sana. Naamini kwamba tume hiyo itaweza kumshauri vizuri ili tuwe na watendaji wazuri katika Wizara hii na katika Mabalozi ambao wataweza kufanya haya tunayoyapanga hapa yatekelezeke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala hili la mapitio ya Sera ya Mambo ya Nje ambayo bado haijakamilika. Na hii ndiyo itakua kioo chetu, hii ndiyo itaweza kutufanya tujipime, kwamba tunakwenda wapi. Kama sera haijakamilika itakuwa pia shida kwamba tunashika lipi na tunakwenda wapi. Kwa hiyo ninashauri kwamba Mheshimiwa Dkt. Tax, uhakikishe kwamba sera hii inapita, ambayo ndiyo itatusaidia katika kuhakikisha kwamba haya yote ambayo tunataka kupitisha leo yanafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika Ripoti ya CAG kuhusu majengo yetu kwenye balozi zetu. Majengo yetu haya yamekuwa ni ya kutia aibu sana. Kwanza, tukumbuke kwamba takriban miaka 50 tulipata viwanja kama kumi hivi kule Zambia tulivyopewa na Hayati Kenneth Kaunda. Viwanja hivyo hata ukifika leo ni mapori. Inatia aibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikwenda Wenyeviti na Makamu Wenyeviti wa Kamati zetu nne; PAC, PIC, LAAC na Bajeti; tulitembelea maeneo yale. Tumeona ni aibu kubwa, maana wale wenye majengo yao, nyumba zao karibu na viwanja vile, kwa kweli wanasikitika sana na wanachukia sana kwamba tumewaachia mapori katika viwanja vile, kwa sababu haviendelezwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hayati Kaunda alikuwa ameona kwamba hii itatusaidia kama vitega uchumi. Na tulipotembelea kule wakati huo aliyekuwa Balozi alituambia kwamba viwanja vyetu kama vingejengwa inavyotakiwa, ni wazi vingesaidia kulipa kodi takriban Balozi zote zilizoko katika Bara la Afrika. Lakini mpaka leo ndiyo tunaambiwa bado bajeti ndiyo inapangwa viwanja hivyo vikajengwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha kusikitisha zaidi ni pale ambapo jengo letu lililopo kule Washington limepoteza kinga ya kidiplomasia kwa kuwa ni chakavu mno, na kwa hiyo wakasema kule wenzetu hatuwezi kuendelea kukaa na uchafu huu, na hatutambui kama ni jengo la Balozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili hiyo tukatakiwa tulipe kodi, na imelipwa kodi kiasi cha milioni 283.3 kwa ajili ya kulipia jengo bovu. Sasa haya ndiyo kati ya mambo ya kujitathmini; hivi kweli tuko serious na tunayoyafanya? Tumeacha kukarabati majengo yetu, tangu miaka 29 Hayati Mkapa alivyosema uchumi wa diplomasia ndiyo utaongoza nchi yetu. Leo majengo tumeyaacha na majengo yale ndiyo ya kututambulisha, kwamba hawa ndio Watanzania. Leo majengo yale yamekuwa ni aibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia pia tuna Balozi 34 ambazo hazina majengo yao. Pamoja na kwamba wamesema 14, angalia hiyo aya 20 yatajengwa lini. Kutokana na hivyo, mwaka 2021/2022 Tanzania ililipa bilioni 15.47 kwa kodi ya mapango haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo unaangalia kwamba hivi kweli diplomasia ya uchumi tunayoongelea maana yake ni nini? Maana yake ni kukuza uchumi. Lakini angalia uone kwamba uchumi wako unaukuzaje wakati una gharama nyingi kuliko ambavyo unaweza ku-sustain hiyo diplomasia ya uchumi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kaboyoka.

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, labda la mwisho, tuna uhaba mkubwa wa uwakilishi wa heshima katika balozi zenye nchi zaidi ya moja. Hilo nalo naomba Wizara iliangalie, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Wanataaluma wa Kemia wa Mwaka 2016
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mimi nitachangia kwa kutaka baadaye nije nipate ufafanuzi zaidi hasa kuhusiana na Chemist Professionals Act.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiangalia majukumu ya Baraza pamoja na mambo mengine ni kupitisha vile vyuo ambavyo vitafundisha hawa ma-professionals. Siku za nyuma tumeona matatizo ya vyuo hivi binafsi ambavyo vimekuwa havifuati maadili na kwa ajili hiyo vimekuwa vinatoa mafunzo na vyeti ambapo watumishi wake wakienda kwenye kazi wanakuwa substandard katika utumishi wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba katika majukumu ya Baraza litusaidie kuangalia vile vyuo vyenye intergrity ambavyo vinaweza kuruhusiwa kutoa hao wataalamu. Nasema hivi kwa sababu vyuo vingine vya binafsi vinapenda vifaulishe na kutoa watu ambao kwa kweli wakienda sehemu za kazi hawafanyi sawasawa na vyeti vile. Nia yao ni kutoa vyeti hivyo ili waweze kuendelea kuonekana wanafanya kazi. Nimeshuhudia sehemu mbalimbali ambapo wataalamu wamekuwa wakitoa majibu ya utafiti waliofanya na kuonesha ni vitu viwili tofauti sana wakati wako qualified.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine nataka nizungumzie matumizi ya hivi vyeti ambavyo hao wataalamu watapewa wakishaandikishwa na Baraza hili. Wataalam hao kwa vile hawako wengi utakuta mtaalam mmoja amejiandikisha katika sehemu tatu au nne za kufanyia kazi na cheti chake kinatumika katika sehemu hizi mbalimbali. Utakuta maabara hasa za hospitali binafsi zinatumia vyeti vya wafanyakazi ambao hawafanyi kazi pale, wamelipwa ili wakija wakaguzi wanaona vile vyeti viko pale na wanaona kweli hii maabara iandikishwe maana ina wataalam na kumbe vile vyeti vilivyotumika wale wataalamu hawafanyi kazi katika maabara zile.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa labda Baraza na Kamati zitakazoundwa zitusaidie kusimamia kanuni za maadili na mwenendo wa wataalamu wawe na uhakiki wa kuonesha kwamba kweli mtaalam ambaye ameandikishwa katika maabara ile ndiyo yuko pale na anafanya kazi pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine ninaloliona katika maabara zetu siyo nyingi, lakini relatively za hali ya juu maana nimepita maabara nyingi kwa sababu zangu mwenyewe, unakuta mkemia yule anayefanya kazi pale anaweza kutumia reagents ambazo zimepitwa na wakati. Mara nyingi hizi reagents zinatumika kwa vile mwenye maabara hataki kupata hasara. Hawezi kusema hapana hizi tusizitumie kwa vile zime-expire matokeo yake zinatoa majibu ya analysis ambayo siyo sahihi. Sasa tujue hizi Kamati zitakuwa na jukumu la ku-inspect kila wakati kuona reagents zinazotumika kufanya analysis katika sampuli mbalimbali zinakuwa hazijapitwa na wakati ili tusitoe majibu ambayo sio sahihi kutokana na reagent ambazo zime-expire. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu kwa vile mara nyingi ina tatizo la ukatikaji wa umeme na reagents nyingine zinatakiwa zikae katika temperature fulani na majenereta ya sehemu zile za kazi hayafanyi kazi zile reagent huwa zinabadilika matokeo yake hata yule analyst akifanya kazi atapata majibu ambayo sio sahihi.
Naomba Kamati hizi zitakazoundwa pamoja na Baraza lenyewe liwe na majukumu ya ziada ya kufanya inspection ambayo ni ad-hock maana tumeshaona wakitoa ratiba kwamba leo wanapita kunawekwa mambo ya ajabu ajabu, wanaletwa wataalam ambao hawapo katika maabara ile na kuoneshwa kwamba yuko pale, siku hiyo zitakuwa displayed reagent ambazo ni nzima na wakati mwingine maabara nyingine wanakodisha vyombo kutoka makampuni mengine inspection ikishapita vile vifaa vya maabara vinarudishwa kwa wenyewe.
Kwa hiyo, ningeshauri Muswada huu pia uzingatie haya ninayozungumza hapa ili utafiti utakaokuwa unafanyika katika maabara zetu na hata tukiwa na wataalam ambao ni wasomi zifanywe kwa uhakika na yapatikane majibu ambayo ni ya kisayansi na sio ya kulipua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.