Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Jacqueline Kandidus Ngonyani (Msongozi) (52 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuwashukuru wanawake wa Mkoa wa Ruvuma kwa kuniamini na kunipa kura za kishindo. Nawashukuru pia wananchi wa Mkoa wa Ruvuma kwa namna ambavyo wamekipa Chama cha Mapinduzi kura za kishindo na hata Majimbo yote sasa ya Mkoa wa Ruvuma ni ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende moja kwa moja kwenye Benki ya Kilimo. Nachukua nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuona umuhimu wa kuanzisha Benki ya Kilimo ili kuweza kuchochea hali ya kilimo katika nchi yetu na kuwafanya wananchi wake waweze kujiwezesha kwa ajili ya kukopa na kuendeleza kilimo mmoja baada ya mwingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na shughuli hiyo inayofanyika kwa maana ya kilimo, naomba niseme tu kwamba katika Mkoa wetu Ruvuma kuna mazao mengi ambayo yanalimwa katika Mkoa huo, lakini leo hii naomba Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Kilimo, aone umuhimu wa kupeleka Benki hii ya Kilimo sasa katika Mkoa wa Ruvuma kwa sababu Mkoa wa Ruvuma ni Mkoa ambao katika shughuli zake asilimia 90 wananchi wote wanategemea kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Benki ya Kilimo ipelekwe huko ili iweze kuwarahisishia wananchi kuweza kukopa na kuendeleza shughuli zao za kilimo, wakiwepo wanawake ambao ni wakulima na wafugaji wanaotokana na Wilaya ya Mbinga, Wilaya ya Nyasa, Wilaya ya Songea Vijijini, Wilaya ya Namtumbo na Wilaya ya Tunduru. Hawa wote wanahitaji wapate pesa kwa ajili ya kuendeleza shughuli za kilimo bila kusahau Halmashauri ya Madaba, nao pia kuna wanawake ambao wanahitaji wapate pesa kwa ajili ya shughuli za kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nisingependa kusema sana kwenye eneo hili, lakini naomba tu endapo Waziri mwenye dhamana atanikubalia kupeleka benki hii kule katika Mkoa wa Ruvuma, azma yangu ya kuondoa shilingi katika bajeti hii nitaiondoa. Vinginevyo nitaondoa shilingi ili anihakikishie kwamba benki hii sasa inakwenda kuhakikisha kwamba wale ambao ndio wanashughulika na shughuli za kilimo, ndio ambao wanasogezewa mahitaji haya. Kwa sababu Benki hii katika Mikoa mitano ambayo ni ya mfano ambao wameanza nayo ni pamoja na Mkoa wa Njombe.
Sasa jamani Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, hivi kutoka Njombe na kufika Songea mbona ni kama pua na mdomo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, pamoja na kazi nzuri anazozifanya, wananchi wanatambua na wana imani kubwa sana na wewe, hasa wananchi wa Mkoa wa Ruvuma, wanawake wa Ruvuma, naomba sana jambo hili ungelitilia mkazo ili tuweze kupata benki na wananchi waweze kufanikiwa kwa ajili ya mahitaji hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Ruvuma pia tunalima mahindi, kahawa na korosho, ndiyo maana ninaona umuhimu wa kusisitiza, kwa maana mazao yote haya ndiyo yanayoipatia pato kubwa sana nchi yetu ya Tanzania. Kwa hiyo, umuhimu wa kupeleka benki ni mkubwa mno.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye suala la zao la tumbaku. Zao la tumbaku ni shida; kila mmoja ameongea hapa! Maeneo mengi sana ni wahanga wa jambo hili. Hata kwetu katika Mkoa wa Ruvuma katika Wilaya Namtumbo kuna shida hiyo. Tunaomba sasa kuhusu gawio ambalo linagawiwa na Wizara kupeleka maeneo ambayo watu wanalima tumbak, basi na Wilaya ya Nambumbo ipewe kipaumbele ili waweze kupata gawio.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika, kwa kuwa mahitaji ya tumbaku duniani yameshuka, ni vizuri sasa Serikali ikajipanga kuhakikisha kwamba zao hili la tumbaku linalimwa hapa hapa ndani ya nchi yetu na wanunue zao hili ndani ya nchi yetu, badala ya kununua tumbaku hii nje ya nchi, kwa mfano, sasa hivi inanunuliwa maeneo mengine ya nje ya nchi ikiwemo Uganda; naomba sana kwa kuwa eneo hili mahitaji yameshuka, basi mazao yatakayozalishwa juu ya suala la tumbaku, nadhani yatakidhi haja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye suala la mawakala wa pembejeo za kilimo. Kwanza kabisa naipongeza Serikali kwa kuona umuhimu wa kupeleka huduma hii ya voucher kwa wananchi wetu, baadhi yao wananufaika na wengine hawanufaiki, lakini najua Serikali yetu ni sikivu, wataona umuhimu wa kufanya marekebisho juu ya jambo hili ili wananchi wote mwisho wa siku waweze kufikiwa na huduma hii. Mawakala wetu kwenye maeneo mbalimbali katika nchi yetu hii ya Tanzania, wamejitoa muhanga kuhakikisha kwamba wameikopesha Serikali kwa kuwapa wananchi pembejeo na baadaye wanakuwa wanaidai Serikali. Wamejitolea!
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuwapongeza sana. Naomba sasa Serikali na Wizara kwa ujumla mwone mchango mzuri ambao mawakala hao wameutoa ili kuwezesha zoezi la utoaji wa voucher uweze kwenda kwa wakati. Kwa misingi hiyo, naomba niwasemee leo mawakala wa pembejeo za kilimo. Waheshimiwa Wabunge wengi waliosimama hapa, mimi naona wamewasahau kabisa kuwasemea; ni watu ambao wamejitoa, lakini mpaka sasa hivi hawajalipwa pesa zao. Wanadai pesa nyingi na wale ni wajasiriamali ambao wanaendesha biashara zao kwa kutumia mikopo mbalimbali; wanakopa kwenye mabenki, SACCOS na maeneo mengine mengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imefika wakati sasa hivi, wale wajasiliamali wamekauka midomo. Hali ni mbaya na wengine wanadaiwa sana na hatimaye wengine tayari wanaweza hata wakafilisiwa mali zao, ikiwemo hata kuuziwa nyumba zao.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wakati unajipanga vizuri kuhakikisha unatekeleza ipasavyo Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwenye eneo la kilimo, naomba uwatazame kwa jicho la huruma sana wajasiriamali waliopo katika Mkoa wa Ruvuma, katika Wilaya zote zinazojumuisha Mkoa wa Ruvuma, tukianza na Tunduru, tukaja Namtumbo, nikaja Songea na hatimaye Mbinga na hata Nyasa. Wote wanahitaji walipwe pesa zao ili waweze kuendelea kujikimu katika maisha yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii niongelee suala la zao la samaki katika Ziwa Nyasa. Naomba nimwambie tu Mheshimiwa Waziri kwamba katika maziwa yote ambayo yanatoa samaki katika nchi hii, hakuna samaki watamu wanaoshinda Ziwa Nyasa. Ziwa Nyasa linatoa samaki watamu sana na wenye virutubisho sana na ndiyo maana ukimwangalia Mheshimiwa Jenista Mhagama, amenawiri, yuko vizuri; ukimwangalia Sixtus Mapunda naye yuko vizuri hata ukinitama mimi niko vizuri kwa sababu ya samaki wazuri na watamu wanaotokana na Ziwa Nyasa. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Uvuvi naomba uelekeze macho yako katika Ziwa Nyasa. Ziwa hili linatoa dagaa wazuri mno haijapata kutokea! Naomba uelekeze nguvu huko! Naishauri tu Serikali kwamba hebu oneni umuhimu... (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika kwanza naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyenzi Mungu kwa kunipa fursa hii ya kuweza kusimama hapa katika Bunge lako Tukufu ili nami niweze kuchangia katika Wizara ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. John Joseph Magufuli kwa kuona umuhimu wa kutenga fedha bilioni 10 kwa ajili kwenda kuboresha makazi ya askari wetu. Hali kadhalika vituo vya polisi vingi vimetengewa fedha kwa ajili ya kuendeleza ujenzi huo na Wabunge wengi wamesimama humu wametoa ushuhuda na mpongeza sana Mheshimwia Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,nimpongeza Waziri mwenye dhama ya Wizara hii ndugu Kangi Lugola unafanya kazi nzuri sana chini ya majeshi yako yote ya Polisi, Magereza, Uhamiaji pamoja na Zima Moto. Ukisikia jirani yako anapiga kelele ujue sindano zinaingia vizuri na unafanya kazi vizuri. Itakuwa ni ngumu sana kwa jeshi la polisi kupewa sifa ya kwamba mnafanya vizuri yaani mpokuwa mnaambiwa hamfanyi vizuri kwa upande wa pili kwamba mpo sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwasihi kwamba kamanda Sirro endelea kufanya kazi sisi wenye nia njema tunaona kabisa kazi unayofanya ni nzuri ulinzi umeimalika katika nchi yetu ya Tanzania watu wamekuwa na nidhamu kazi zinafanyika kwenye maeneo mbalimbali hata vijana waliokuwa wanashinda vijiweni vibaka nao pia wamepungua sana hongera sana kama Sirro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la kasma ya mafuta kwa jeshi la polisi, magereza na maeneo mengine. Pesa imekuwa inatengwa kidogo kuelekea kwenye maeneo hayo ili waweze kutimiza shughuli zao. Inafika kwa muda mfupi sana unakuta pesa inaisha wanashindwa kutimiza wajibu wao. Kwa hiyo, naomba majeshi haya yote yatengewe fedha ili waweze kufanya shughuli zao kwa maana ya kupata mafuta yanayotosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kasma ya vipuli magari yameongezwa nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kuongeza magari katika jeshi la polisi. Lakini pia vipuli navyo viongezwe kwa sababu vipuli bado ni vichache kwa hiyo wanashindwa kufanya mategenezo pale inapotokea magari yanapata uharibufu.

Mheshimiwa Spika, zipo stahiki za maskari ambazo wanashindwa kuzipata kwa mfano kuna suala plain clothes ambalo ni allowance kwa ajili ya CID. Hii allowance hawaipati kwa hiyo nilikuwa naomba sana watengewe fedha kwa ajili ya kupata hiyo allowance ili waweze kufanya kazi yao vizuri. Lakini pia kuna house allowance, house allowance inatakiwa 15% ya mshahara wa kila askari lakini hawapati kwa hesabu hiyo ya 15% naomba wapigiwe kwa 15% ili waweze kupata allowance hiyo.

Mheshimiwa Spika, mafao ya askari polisi, askari polisi wamekuwa wakipata mafao lakini hayo mafao yanachewa sana, siku za nyuma walikuwa wanatumia karibu mwaka mmoja na nusu ili waweze kupata mafao baada ya kustaafu. Lakini sasa hivi imepungua walau mwaka mmoja. Niombe Serikali ipunguze zaidi sababu askari wetu wanapokuwa wamestahafu kuendelea kukaa katika hali ya manung’uniko hawapati fedha zao kwa wakati nayo pia haileti tija kwa sababu kazi yao ni gumu na wanafanya kazi pia wakati mwingine katika mazingira magumu wamapate fedha zao kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, lakini pia hawa askari inapotokea askari amefariki wanaobaki ndugu zao kuhusu suala la mirathi wanapata shida sana wanatumia muda mrefu sana kupata mirathi ya ndugu zao. Kwa hiyo, naomba sana Serikali izingatie suala hili hasa pale tunapojua kwamba umuhimu wa jeshi la polisi kama ambavyo Wabunge wengine wamezungumza humu kwamba jeshi la polisi linafanya kazi nzuri na sisi tumo humu ndani kwa utulivu kwa sababu jeshi la polisi linafanya kazi yake barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie pia suala la fidia kwa askari magereza na askari polisi. Inapotokea kwa majeshi haya inapotekea amepata madhara kazini, ameumia kazini sheria ya tume ya polisi namba 25 inaeleza kwamba askari huyu baada ya kuumia alipwe pesa apate fidia. Lakini haielezi kwamba fidia ile anayoilipwa inatoka katika fungu gani? Sasa leo hii naomba nishauri Serikari yangu, kwamba kwanini Serikali isikae pamoja na jeshi la polisi wakazungumza na wakaweza kuchukua utaratibu wa hawa askari wote wakaunganishwa kwenye mfuko wa fidia badala ya hawa askari baada ya kupata matatizo wanajikuta kwamba wanasubiri yale mafao ambayo hayajulikani yanatoka fungu gani ni mpaka waombe benki kuu. Kwa hiyo, naomba sana suala hili lisimamiwe na lizingatiwe.

Mheshimiwa Spika, askari wetu hawa nao pia ni binadamu, ambao wameumbwa kwa mfano wa kila binadamu hapa ndani kwa maana ya Mungu. Hawa askari hawana moyo wa chuma wana moyo wa kibinadamu, wana moyo wa nyama.

Mheshimiwa Spika, inapotokea mtu anasimama humu katika Bunge lako hili Tukufu anawatuhumu askari. Jana amesimama Mbunge mmoja humu ndani akazungumzia suala la askari kuwabaka, kuwalawiti wanawake wanaokwenda kwenye vituo vya polisi. Miongoni mwa vituo ambavyo alivitaja ni pamoja na kituo cha Mtakuja Dar es Salaam na Staki shari na vingine lakini miongoni mwa hivyo. Sasa najiuliza ni kweli askari hawa wanafanya vitendo vya aina hii? Na kama ndivyo ni kwa nini aleze kwa maana askari wote…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JACQUELIN N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, na kama ndivyo kwa nini asichukuliwe akatoa ushahidi?

SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa taarifa yangu kwanza nisikitike, anayechangia ni mwanamke. Jana nimechangia nikasema mabinti wanabakwa, wanatendewa kinyume na maumbile wanaambukizwa na UKIMWI niseme tu hii sio mara ya kwanza nimeongelea Bungeni. Alikuwa anakuja RCO kutoka Kanda Maalum gerezani tulimueleza na mifano. Nilipotoka tu gerezani niliongea na waandishi wa habari nilisema sasa ukiona Mbunge anabisha badala kwenda kusema!

SPIKA: Ulisema kwamba?

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, kwamba kuna mabinti wanatendewa ndivyo sivyo na wapo wanabakwa, wanaingiliwa kinyume na maumbile wanaambukizwa na UKIMWI na nikataja maeneo ya vituo ambavyo wametaja, na walivyokuja gerezani walisema wanaenda kufuatilia. Sasa na RCO kutoka Kanda Maalum sasa ukiona Mbunge ambaye amekuja kuwatete wananchi anatetea vitu anapindua, inabidi aombewe na inasikitisha sana. Polisi nimetoa taarifa ni chombo ambacho tunaongea huku Bungeni, wataeenda watafuatilia wataona the validity ya hiyo kitu na sio vinginevyo. Naomba sana Bunge hili litumike kushauri na kukemea na sio kutetea. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana, nafikiri ulikuwa unampa taarifa

MHE. ESTHER N. MATIKO: Kama mnawapenda polisi mgeweza kubadilisha hata leo bajeti tukaingoza tukawajengea majumba wanateseka au tukawaongezea mshahara.

SPIKA: Ahsante sana inatosha Mheshimiwa Msongozi unapokea taarifa hiyo!

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ninayezunguza ni Mwanamke na nina uchungu na wanawake wenzangu na walionileta ndani ya humu ndani ya Bunge hili ni wanawake. Siwezi kufurahia mwanamke mwenzangu analawitiwa, amekuwa na haraka ya kuyadaka maneno kabla ya kusikiliza nini ninachokisema angesubiri akaona concern yangu nini. Nasikitika sana kwa kudaka daka maneno. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nataka niseme hivi, huyo Mbunge ambaye ameeleza habari hii kama kweli vitendo hivyo vipo awataje hao polisi wanaofanya hivyo ili waweze kuchukuliwa hatua, kwa sababu vitendo hivyo kwa wanawake wenzetu sisi hatukubaliani kama wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini isiwe kwamba Askari wote wanapakwa matope hayo, a-specify ni nani na nani? Ina maana kwamba leo hii kwa watu ambao wamesikiliza ile clip wanawake wote wataogopa kwenda kwenye Vituo vya Polisi, wanaogopa kubakwa na kufanyiwa vitendo vya ulawiti. Kwa hiyo, a-specify. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naomba hili suala lisichukuliwe kimzahazaha asaidie Polisi ili kutoa ushuhuda wa kina ili Polisi na Serikali walifanyie kazi kwa sababu mwisho wa siku isiwe ni katika hali ya udhalilishaji kwa Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme hivi, nakubaliana na wale wote ambao hawakubaliani na suala la maandamano, lakini pia hawakubaliani na suala la mikutano holela holela. Sisi kama Wabunge ziko kazi tumepewa na wananchi kwenda kuzifanya. Nashangaa sana Mbunge anasimama hapa, toka lilianza Bunge yeye anazungumzia maandamano tu. Naweza nikafananisha na mnyama mmoja anaitwa nyumbu.

Mheshimiwa Spika, tabia ya mnyama anaitwa nyumbu anafanana hivi; mmoja akiongoza njia kwenda, basi wote wanakwenda huko hata kama kule kuna samba, wote wataelekea huko; hata kama kuna shimo, wote wataelekea huko. Sasa hivi humu ndani ya Bunge hamna agenda nyingine, ni kuongelea tu suala la maandamano, suala la Askari wamefanya nini.

Mheshimiwa Spika, suala la mikutano nasema nampongeza Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, mikutano yote isiyokuwa na tija ikomeshwe. Hakuna mikutano, watu wakafanye kazi. Watu walikuwa wamezoea kuchukua vijimambo vidogo vidogo, anabeba kama dili anaenda nalo kwenye mkutano kupotosha watu na kufanya mambo yasiyostahili.

Mheshimiwa Spika, naomba sana nipongeze Jeshi la Polisi, Kamanda Sirro kazia hapo hapo, endelea kufanya kazi yako, tuko nyuma yako. Sisi tutakutetea na tutakusaidia.
(Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, tunataka nchi iwe na amani, nchi iwe na utulivu badala ya watu kufanya mambo yao binafsi.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Jacqueline Msongozi.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja asilimia kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kutoa pole sana kwa familia ya aliyekuwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, ambaye alifariki dunia tarehe 17 ya mwezi wa Tatu. Natoa pole nyingi sana kwa familia, pole nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan; pole sana kwa Waziri wetu Mkuu; viongozi wengine wote na wananchi wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Jemedari, mwanamke shupavu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mwenyezi Mungu amjalie kila kheri ampe kila namna iwezekanayo ili aweze kusimama imara katika uongozi mzima wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, leo nina mambo matatu tu ya kuchangia katika Mpango huu wa Maendeleo. Nianze na suala nzima la Sekta ya Kilimo. Mara nyingi sana nimekuwa nikisimama hapa ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nazungumzia sana suala la kilimo hasa tunapokwenda kufungamanisha kilimo na masuala mazima ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri shahiri, pasipo shaka yoyote, bila kuimarisha Sekta ya Kilimo hatutaweza kufikia malengo tunayokusudia katika mpango mzima wa kukuza uchumi katika nchi yetu ya Tanzania. Hivyo basi, naomba Serikali yangu sikivu kwamba mpango huu wa kilimo uende sambamba na kuhakikisha kwamba masuala mazima ya mbegu kuelekea katika uwekezaji kwenye kilimo kuwe na mpango Madhubuti, yaanzishwe mashamba ambayo yataweza kuandaa mbegu nzuri ambazo zitauzwa kwenye maeneo mbalimbali kwa bei nafuu ili uwekezaji huu ufanyike na uwe na tija kwa Taifa na pia katika kuinua masuala mazima ya kiuchumi katika nchi yetu na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, suala la kilimo ni lazima pia liambatane na masuala mazima ya masoko. Masoko imekuwa ni tatizo. Uwekezaji ni mkubwa sana unaofanywa na wananchi wakitumia nguvu nyingi na wakati mwingine wananchi wanafanya kazi kwa kutumia mikono yao, hawana hata zana za kilimo zilizo bora ili kuweza kuwezesha Sekta hii ya Kilimo na uwekezaji wao.

Mheshimiwa Spika, pia kumekuwa na tatizo la masoko, masoko ni tatizo. Mkulima alime mwenyewe na atafute soko mwenyewe. Naomba sasa Serikali yangu kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara wajipange vizuri kuhakikisha kwamba wanatafuta masoko ili wawekezaji wetu kwenye masuala mazima ya kilimo wafanye uwekezaji wenye tija.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, kumekuwa na mikoa ambayo imekuwa ikizalisha sana mazao ya nafaka ambayo kimsingi inasaidia sana katika kuweka uimara na kuhakikisha kwamba tunakuwa na akiba nzuri ya chakula. Unapoitaja mikoa hiyo, huwezi kuacha kuutaja Mkoa wa Ruvuma ambao umeshika nafasi ya kwanza mara nne mfululuzo katika uzalishaji wa mazao ya nafaka, ukifuatiwa na Mkoa wa Songwe, unafuatiwa na Mkoa wa Rukwa na mikoa mingine.

Mheshimiwa Spika, mikoa hii inafanya vizuri sana. Sasa endapo kama mikoa hii inafanya vizuri, itoshe tu leo niongee mbele yako dhidi ya Waziri wa Fedha aweze kutoa tunu kwa mikoa hiyo kwa kupeleka Benki ya Kilimo. Benki ya Kilimo hiyo itafanya uwekezaji maeneo hayo ili waweze kuwakopesha. Pia iende sambamba na mikoa mingine inayolima pamba, Mkoa wa Dodoma unaolima zabibu na maeneo mengine yote ambayo katika nchi yetu yanafanya vizuri waweze kwenda kupelekewa Benki ya Kilimo ili iweze kuwasaidia wananchi katika kuwainua zaidi kwa sababu wananchi bado wanauhitaji, lakini wanapata wapi mitaji ili wawekeze vizuri zaidi kwenye kilimo. Unakuta Benki ya Kilimo ipo pale Dar es Salaam inashangaa shangaa tu, nani anayelima pale Dar es Salaam. Ni vizuri basi Waziri wa Kilimo apeleke Benki hizi kwenye maeneo husika yanayofanya vizuri ili weweze kuwainua kiuchumi na waweze kufanya uwekezaji mzuri katika masuala mazima ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, sasa naenda kwenye suala la barabara; tumekuwa tukizungumza sana kuhusiana na masuala ya barabara. Lengo ni kuhakikisha kwamba maeneo yote ya nchi yetu ya Tanzania yanafunguliwa na barabara zetu zikiwemo barabara za kawaida ambazo zinasimamiwa na TARURA, lakini pia zikiwepo barabara ambazo zinasimamiwa na TANROADS ili kuweza kurahisisha uchukuzi na kurahisha uzalishaji ambao utapelekea ukuaji wa kasi wa uchumi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sasa hapa naomba niende moja kwa moja kwenye suala la PPP (Public Private Partnership). Suala hili na wewe umelidokeza hapo, ni jambo zuri kabisa, Serikali isijilimbikizie miradi mikubwa kuhenyeka nayo, kutabika nayo, badala yake wafungue fursa ili taasisi na mashirika mbalimbali na sekta binafsi zinazoweza kuja kuwekeza basi zije kuwekeza katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, Sheria Na. 18 ambayo ilifanyiwa marekebisho katika Bunge lako Tukufu hili mwaka 2010, sheria hii haijamnufaisha mwananchi wa Tanzania, bado sheria hii haijamnufaisha mwanaumma wa Tanzania. Nasema hivi kwa sababu sheria imefanyiwa marekebisho kwamba sekta binafsi sasa ziungane na Serikali ili kuweza kutanua wigo na waweze kuwekeza kwa maslahi ya Watanzania, lakini bado sheria hii haijafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, unakumbuka tarehe sita Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amelihutubia Taifa akiwa anaapisha watendaji mbalimbali pale Ikulu, ameeleza Mama samia na ameonesha dhahiri pasipo shaka kwamba anahitaji sekta binafsi zije ziwekeze katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, sasa ni wajibu wa viongozi mbalimbali wanaohusika katika sehemu mbalimbali kuweza kutoa ushirikiano ili wawekezaji hawa waweze kuja na kuwekeza ili sheria hii Na. 18 iliyorekebishwa mwaka 2010 iweze kufanya kazi na kuleta tija kwa Watanzania ambayo itasababisha ukuaji wa uchumi. Wawekezaji hao watalipa kodi, lakini itaongeza ajira na pia itainua uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, utengenezaji wa barabara; nakumbuka mwaka 2017 ulinipa fursa ya kwenda Nchi ya China kikazi kwa majukumu ambayo ulitupa sisi kama Wabunge wako, tulikuwa Wabunge 20. Nilijifunza jambo kubwa sana na Mungu akubariki sana wakati mwingine sasa naomba unipe fursa hiyo kwa nchi nyingine, nitakuja na mchango hapa ndani ya Bunge. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, jambo nililiona China mwaka 2017, leo hii ninachangia ndani ya Bunge kwamba niliona kuna barabara ambazo zimetengenezwa kwa mtindo wa PPP ambazo zimekuwa zikisaidia sana katika Nchi ya China ambayo miundombinu ya barabara imezagaa kila mahali. Vile vile imekuwa ikisaidia pato la nchi linaendelea kukua na wananchi walioko wanaendelea kunufaika na kurahisha shughuli zao za kuendeleza uchumi.

Mheshimiwa Spika, hukunipeleka bure kule, nimepata hiyo exposure na leo nasimama ndani ya Bunge lako Tukufu kuweza kuchangia hilo na kwamba kuona kwa macho.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani kwamba….

SPIKA: Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Msongozi anasema kwamba fursa ya Waheshimiwa kutembeatembea kidogo ina faida. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Jacqueline malizia dakika zako.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, sasa hili suala la PPP kwenye barabara zetu tungeweza kuchukua watu wa NSSF wakatengeneza barabara hapa na zikawa zinalipiwa, Serikali inapata mapato yake, NSSF watapata mapato yake na pia wananchi watapata ajira na nchi yetu itaendelea kiuchumi. Hali kadhalika tunahangaika hapa kuzungumzia barabara za kufungua baina ya nchi na nchi, kwa mfano kuna barabara yetu ya Likuyufusi - Mkenda ambayo inaungana na Nchi ya Mozambique. Barabara hii ikitengenezwa kwa mtindo wa PPP itasaidia sana kurahisisha kufungua uchumi huo.

Mheshimiwa Spika, pia kuna barabara ambayo ipo Kakonko barabara hiyo ina urefu wa kilimita 40, inatoka Kakonko halafu inakwenda Muhange. Kwa hiyo hii barabara ingeweza kufungua na mahali pale nimekwenda wakati wa kampeni, nimekuta wananchi wa eneo hilo wana soko kubwa sana pale. Kwa hiyo ikiunganishwa hii barabara na wananchi wale wakawa wana zile movements za kulipia hiyo barabara, ni wazi kwamba Serikali itaongeza mapato makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye suala la tatu na la mwisho, sasa nizungumzie uwezeshaji wanawake kiuchumi, mama ni mama tu, kwa kweli ukimwezesha mwanamke umewezesha familia na umewezesha jamii kwa nzima kwa ujumla. Wanawake wamekuwa wakiwezeshwa kupitia halmashauri zetu mkopo wa asilimia 10 kwa mgawanyo wa 4, 4, 2. Halmashauri zingine hazina uwezo wa kuwakopesha wanawake hawa wakaweza kufanya uwekezaji wenye tija kwenye maeneo yao. Sasa niiombe Serikali yangu tukufu iweke utaratibu mzuri ambao utasaidia wanawake wengi kukopeshwa wakiwepo wanawake wa Jimbo la Kongwa, kule Kongwa wanawake wale wakiwezeshwa vizuri kwa vyovyote vile hata familia zao zitaimarika zitaboresheka na mambo yatakwenda barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho suala la mifugo,

SPIKA: Ahsante, muda umekwisha.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. JACQULINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Kwanza kabisa nianze kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, Serikali imara, yenye Sera nzuri zinazokubalika na zinazotekelezeka. Niipongeze sana Serikali yangu ya Awamu ya Nne iliyokuwa ikiongozwa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Katika Wizara hii ya Miundombinu ilikuwa na Jemedari wetu ambaye sasa hivi ni Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dkt. John Pombe Magufuli. Serikali hii imefanya kazi nzuri ya kuhakikisha ya kwamba mikoa yetu inaunganishwa na barabara za lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inashangaza sana hata kama huna masikio, lakini hata macho hayaoni? Amesimama mlevi mmoja hapa, mimi namuita mlevi, amesimama mlevi akisema kwamba eti Serikali ya Chama cha Mapinduzi hamna chochote inachokifanya. Barabara hizi zimejengwa kwa 31% kwa miaka 15! Safari ni hatua, kama imefikia 31% ina maana Serikali inafanya kazi na inaendelea kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumtia moyo Waziri wa Miundombinu na Naibu wake pamoja na delegation yake yote, endeleeni kuchapa kazi, sisi tuko nyuma yenu, tunaendelea kuwaombea. Kazi mnayofanya ni nzuri na inaendelea kuonekana kwa hiyo, ungeni pale ambapo Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na Dkt. Magufuli walipoishia ninyi endelezeni pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niseme tu kwamba, hakuna mwanamke yeyote yule atakayeweza kumsifia mke mwenzake hata siku moja. Mke mwenza ni mke mwenza tu na kama ikitokea ukamsifia mke mwenzako basi wewe kidogo utakuwa fuse down. Hali kadhalika, debe tupu ndilo lenye kelele, debe lililokuwa na ujazo mzuri halipigi kelele. Tunawashukuru wananchi wetu wa Tanzania ambao wameona umuhimu wa kukipa Chama cha Mapinduzi kura za kishindo na wakiwa na imani na Serikali yao kwamba ina sera nzuri na zinazotekelezeka na sasa hivi Chama cha Mapinduzi kiko mtamboni kitaendelea kutekeleza majukumu yake. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye nyumba za Serikali. Nyumba za Serikali zilizokuwa zinasemwa hapa ni nyumba ambazo ziliuzwa wakati wa Rais wa Awamu ya Tatu akiwepo Waziri Mkuu ambaye ndiye mwaka jana alikuwa miongoni mwa watu wa mabadiliko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Sumaye ndiyo ambaye alikuwa Waziri Mkuu kwa wakati huo na ndiye aliyesimamia. Kama alifanya kazi mbaya basi muone kwamba mabadiliko mliyokuwa mnaenda kuyafanya ni mabadiliko hovyo…
MHE. JACQUILINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwasababu hata ambaye alipewa ridhaa ya kuipeperusha bendera ya CHADEMA kwa mwaka jana naye ni hovyo, fisadi aliyepindukia na pia ukija na Mheshimiwa Sumaye naye ni tatizo! Ndiye aliyeuza nyumba hizo kwa mipango mibovu!
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisiharibiwe muda kwa sababu sindano zinapoingia na wao watulie kama wao walivyokuwa wanaingiza sindano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua lazima Wananchi watambue wazi kwamba, hata katika suala ambalo kwa mfano tunachangia humu ndani, upande mwingine ni kelele maana yake ni madebe matupu na upande mwingine wanatulia kwa sababu wana hoja. Na niseme tu kwa upande wa wenzetu wa Upinzani kwa wanawake wanaoweza kujenga hoja ni watu wawili, Mama Sakaya na Upendo, lakini wengine the rest hamna kitu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye hoja ya msingi sana. Pamoja na kazi nzuri ambayo inaendelea kufanywa na Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, naomba niende moja kwa moja kwenye barabara yenye urefu wa kilometa 124, barabara ambayo inatoka Likuyufusi kuelekea Mkenda. Barabara hii ni ya muda mrefu, Waheshimiwa Wabunge waliopita, Mheshimiwa Jenista Mhagama, dada yangu Stella Manyanya na Marehemu John Komba na wengineo walisimama imara sana kutetea hii barabara ili iweze kujengwa, lakini mpaka sass hivi barabara hii haijajengwa, ni barabara ambayo inaunganisha Msumbiji na Tanzania. Naomba Waziri mwenye dhamana, barabara hii iweze kuanza kujengwa kwa kipindi hiki cha mwaka 2016/2017, utakapokuja hapa wakati una-wind up tafadhali naomba ueleze bayana barabara hii inaanza lini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye barabara ya Morogoro - Ruvuma; mimi hizo kelele hazinibabaishi kwa sababu ninyi kwetu, kwa lugha ya kwetu tunawaita mazindolo. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ambayo inaunganisha mkoa wa Morogoro na mkoa wa Ruvuma, na sisi kwetu hatuna aibu Wangoni hawana aibu hata kidogo kwa hiyo, barabara hiyo inatoka Kidatu – Ifakara – Lupilo – Malinyi – Londo – Lumecha mpaka kufika Songea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kwa kifupi nichangie hotuba ya Waziri wa Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukataji miti hovyo ni chanzo kikubwa sana kinachochangia mabadiliko ya hali ya hewa ikiwa ni pamoja na nchi yetu kuelekea kuwa jangwa. Uchomaji wa mikaa hovyo nao pia unachangia sana mabadiliko ya hali ya hewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na uharibifu mkubwa sana juu wa vyanzo vya maji kutokana na matumzi mabaya ya ardhi. Kwa nini:-
(a) Halmashauri zetu zinaruhusu wananchi kujenga ndani ya vyanzo vya maji, sheria ifuate mkondo wake.
(b) Uchimbaji wa mchanga na kokoto navyo vinachangia uharibifu wa vyanzo vya maji, sheria ifuate mkondo wake.
(c) Shughuli za kilimo ndani ya vyanzo vya maji nalo ni tatizo kubwa, sheria ifuate mkondo wake.
(d) Shughuli za ufugaji ndani ya vyanzo vya maji zidhibitiwe ili vyanzo vyetu visiendelee kuharibiwa.
(e) Tusiruhusu nchi jirani kuingiza mifugo katika nchi yetu, ni hatari sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono michango ya TANAPA kwa jamii na nawapongeza kwa dhati na niombe taasisi au mawakala wengine wa Serikali kama TANAPA watoe mchango kwa jamii kama TANAPA wanavyofanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko ya hali ya hewa. Hili ni janga la kidunia, tukiwa kama nchi ambayo ina misitu na maliasili nyingi yafaa tuendelee ku-maintain misitu, uoto wa asili, vyanzo vya maji, tusichanganye mifugo na wanyamapori kama ambavyo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakichangia kwamba maeneo ya hifadhi nao wachunge ng‟ombe. Napinga vikali jambo hilo, tena nasisitiza sana kuwa sheria itumike ili waamue kupunguza mifugo na wakipunguza mifugo watafuga kwa tija badala ya sasa ng‟ombe kibao lakini ukiwatazama ng‟ombe hao wana uzito sawa na bata. Ni wazi kuwa ng‟ombe huyu hatamsaidia mfugaji, ni kero.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wa kiwanda cha Baraghashi – Sao Hill. Hiki kiwanda kinapata gawio la misitu 60% bado wanapata bei punguzo. Jambo la kusikitisha ni kwamba kiwanda hiki kinazalisha karatasi ngumu, anasema finishing anakwenda kufanyia Kenya, jambo ambalo sio kweli, anachokifanya huyu mwekezaji ni kukwepa kodi ya Serikali. Nashauri afuatiliwe kwa ukaribu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) wafanye kazi yao badala ya kujiingiza kwenye biashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja asilimia mia moja na naomba mchango wangu uingie kwenye Hansard.
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii nami nichangie Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa 2016/2017. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge hili, nachukua nafasi hii kuwashukuru sana wanawake wa Mkoa wa Ruvuma ambao walinipa kura za kishindo ili niweze kuwawakilisha vyema katika vikao hivi vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nawashukuru sana wanawake wenzangu wa Mkoa wa Ruvuma.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nachukua nafasi hii kuwashukuru wapigakura wote wa Mkoa wa Ruvuma ambao wamehakikisha kwamba Chama cha Mapinduzi kinashinda Majimbo yote ya Mkoa wa Ruvuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye suala la umeme. Kwa kuwa kwenye Mpango huu kimsingi tumejipanga kuhakikisha kwamba tunakua kiuchumi hasa kupitia viwanda; na kwa kuwa viwanda vyetu haviwezi kuendeshwa bila kuwa na umeme wa uhakika; sijaona mpango mzuri ambao umewekwa kuhakikisha kwamba umeme wa grid ya Taifa kutoka Makambako kuelekea Songea unasimamiwa vizuri ipasavyo na kuhakikisha kwamba mradi huu wa umeme unatekelezwa kwa haraka ili kurahisisha ujenzi huu au Mpango huu wa Viwanda ambao Taifa kwa ujumla limejipanga hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mashaka yangu ni kwamba, inawezekana kabisa Mkoa wa Ruvuma tukaachwa nyuma kwa kuwa bado umeme huu wa grid ya Taifa haujafika huko. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri wa Nishati ahakikishe kwamba katika bajeti hii, suala la kuhakikisha kwamba umeme wa grid ya Taifa unafika Mkoani Ruvuma ni muhimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, naomba nizungumzie suala la maji. Kwa kuwa suala la maji ni muhimu sana katika ustawi wa maisha ya binadamu hasa wananchi wetu na kwa ujumla nchi nzima, naomba leo niongelee eneo moja la shida ya maji ambayo inaukumba Mkoa wa Ruvuma. Katika Wilaya ya Tunduru, Namtumbo, Songea Mjini, Songea Vijijini, Madaba, Wilaya ya Nyasa pamoja na Wilaya ya Mbinga, kiukweli kuna shida kubwa sana ya maji. Katika Mpango huu wa utekelezaji wa mwaka 2016/2017 sijaona mkakati madhubuti ambao utapelekea kupunguza adha ya maji kwa wanawake wa Mkoa wa Ruvuma.
Kwa hiyo, nadhani ni vizuri Wizara hii ya Maji ione umuhimu katika kuhakikisha kwamba endapo hakutakuwa na uwezekano wa kupata maji ya mtiririko kwa mwaka huu, basi wanawake wale waweze kuchimbiwa hata visima virefu wakati wanaendelea kusubiri mpango wa maji ya mtiririko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, kimsingi Wilaya zote za Mkoa wa Ruvuma zina shida hiyo na wanawake wa Mkoa wa Ruvuma ni wanawake ambao ni wajasiriamali, lakini pia ni wakulima. Kwa hiyo, wanatumia muda mwingi sana kwenda kufanya shughuli ya kutafuta maji badala ya kwenda kufanya shuguli zao za kilimo na hata nyingine za ujasiriamali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee pia suala la bandari kama Mpango ulivyoainisha suala la kuboresha bandari. Katika Wilaya ya Nyasa tuna ziwa Nyasa lakini pia kuna gati la Ngumbi. Zabuni ya ujenzi wa Gati ya Ngumbi ulikamilika tangu Januari, 2015, lakini ujenzi mpaka sasa hivi haujaanza na wala hakuna matumaini yoyote. Katika Mpango huu sijaona kama kuna fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya mwendelezo huo, ni maneno tu yanaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kwamba Mpango huu wa ujenzi wa Gati hii ni wa muda mrefu sana takribani miaka 20 sasa. Kwa kuwa katika Mpango huu pia bado halijaingizwa hili suala, ni mashaka yangu kwamba inawezekana tunaingiza vitu kwa maana ya mpango lakini utekelezaji unakuwa sivyo. Naomba sana, Gati hili la Jimbo la Nyasa litengewe fedha kwa ajili ya utekelezaji na siyo maneno. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala la kilimo. Mkoa wa Ruvuma ni Mkoa ambao unashika nafasi ya nne Kitaifa kwa suala la kilimo. Pamoja na mazao mengi yanayozalishwa katika Mkoa wa Ruvuma, lakini leo naomba niongelee zao ambalo linazalishwa katika Wilaya zote za Mkoa wa Ruvuma ambalo ni zao la mahindi. Hili ni zao la chakula katika Mkoa wetu lakini pia ni zao la biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Mpango Mzuri wa Serikali wa kuhakikisha kwamba unatoa Ruzuku ya Serikali kwa ajili ya pembejeo za kilimo kwa maana ya voucher, niseme tu kwamba vouchers hizi kimsingi hazimnufaishi mwananchi wa kawaida wa pato la chini. Badala yake kumekuwa na vurugu, yaani kutokuelewana baina yao wenyewe; wananchi wao kwa wao pamoja na wanaosimamia. Tatizo ni kwamba voucher ni kidogo na hitaji ni kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nafikiria kwamba ni vizuri basi Mpango huu wa Serikali ungekuja na Mkakati maalum namna gani unamwezesha mwananchi ili aweze kupata pembejeo za kilimo kwa bei nafuu baada ya kuondoa kodi ili kila mwananchi aweze kuchukua pesa yake kununua pembejeo za kilimo kwa bei nafuu badala ya kuwa baadhi wanapata voucher na wengine hawapati. Matokeo, mnatusababishia ugomvi ambao siyo muhimu kwetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nadhani Mpango huu ungekuja na Mkakati wa kuona namna gani kodi inaondolewa na wananchi wale waweze kufikiwa, mmoja baada ya mwingine aweze kujikimu mwenyewe kununua pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Mpango Mzuri wa Serikali wa kuhakikisha kwamba wananchi wanawezeshwa kwa maana ya Shilingi milioni 50 kila Kijiji na kila Mtaa, ni mpango mzuri sana wa kuhakikisha kwamba uchumi wa mwananchi mmoja mmoja unakua. Naipongeza sana Serikali kwa kuona umuhimu wa kufanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mpango huu pia sijaona mkakati madhubuti ambao umewekwa kuhakikisha pesa hii inayoenda kwa ajili ya kumwinua mwananchi mdogo, inatengeneza mazingira ya kumwondolea kodi zisizokuwa za lazima au ushuru usiokuwa wa lazima.
Mheshimiwa Naibu Spika, pesa hii inalenga kabisa kuwainua watu wafuatao: kwa mfano, vijana, mama lishe, bodaboda, wauza matunda na wauza mboga mboga. Sasa ushuru ambao wanatozwa kwenye masoko yao ni ushuru mkubwa. Haiwezekani mtu ana fungu tano za nyanya anatozwa Sh. 1,000/= kutwa! Hiyo ni shida! Kwa hiyo, Mpango huu uende na mkakati wa kuona ni namna gani wataondoa huo ushuru usiokuwa na umuhimu ili kumfanya mwananchi huyu, kweli kile anachokipata aweze kukizungusha na kujikimu katika maisha yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la Benki ya Kilimo. Ni jambo jema Serikali kuanzisha Benki hii ya Kilimo, lakini ndani yake nimeona kuna vitu ambavyo siyo sahihi. Benki hii imeanzishwa kwa madhumuni ya kumwinua mkulima, lakini kwenye utekelezaji iko ndivyo sivyo kwa sababu zifuatazo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma vizuri kwenye mapendekezo ya Mpango huu na nimeona kwamba kuna baadhi ya mikoa ambayo imetengwa kwa ajili ya majaribio na imeshaanza kupelekewa fedha. Baadhi ya hiyo Mikoa ni Iringa; sina shida, wananchi wa Iringa wanalima, lakini pia Mkoa wa Njombe sina tatizo nao, wanalima vizuri tu; Mkoa wa Morogoro nao pia ni wakulima wazuri; hata Pwani, wanalima.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vitu vya kushangaza sana eti Mkoa wa Dar es Salaam nao umepangwa kwa ajili ya watu kupata pesa ya kilimo. Jamani, tuseme ukweli, hivi Dar es Salaam kuna mashamba ya kulima? Mbona hatujaona hayo mashamba, wanalima wapi? Ina maana kuna mashamba Mikocheni, Oysterbay na hapo Sinza Mori? Haya ndiyo mambo ambayo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hayataki na ndiyo anayamulika. Haya ni sehemu ya majipu. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kweli Serikali imejipanga kumwinua mkulima wa kawaida wa hali ya chini, ni vizuri basi malengo haya yakaenda moja kwa moja kwenye maeneo ambayo wananchi wapo na wanalima kweli, badala ya kwenda kuwanufaisha tu watu wamekaa tu maofisini, wengine wamekaa kwenye magari yao, full viyoyozi, wanapata pesa za kilimo ilhali hawalimi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niongelee kuhusu suala la Uwekezaji. Mpango wa Serikali juu ya suala la uwekezaji naona ni mzuri, lakini pia nadhani uende sambamba na kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo yalikuwa yamechukuliwa na Serikali kwa ajili ya kuendeleza viwanda kwa maana ya ardhi ya wananchi ambayo imechukuliwa, basi Mpango huu wa Serikali wa kuendeleza viwanda uende sambamba na kulipa fedha za fidia kwa wananchi ambao wamechukuliwa maeneo yao, ikiwemo eneo la Mwenge Mshindo katika Wilaya ya Songea Mjini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu sana wawekezaji hawa EPZ wamechukua maeneo makubwa sana ambayo mpaka sasa hivi inakaribia miaka 15 au 16 wananchi hawajalipwa pesa zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba….
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha.
MHE. JACQULINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo naomba kwenye suala la miundombinu, barabara inayotoka Makambako kwenda Songea…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ngonyani!
MHE. JACQULINE N. MSONGOZI: Nayo pia ifanyiwe marekebisho ni mbaya sana.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ngonyani, muda wako umekwisha.
MHE. JACQULINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya TAMISEMI.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua nafasi hii pia kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri ambayo anaifanya na anaendelea kuifanya. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kazi nzuri anayoifanya ya kusimamia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze pia Mawaziri wote kwa Wizara mbalimbali kwa jitihada zote ambazo mnaendelea nazo kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Hongereni sana, kazi mnayofanya inaonekana na Mungu awajaalie kila la kheri, awape wepesi ili muendelee kudunda kazi kama kawaida. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo nimeona ni vizuri nikaenda moja kwa moja kwenye eneo la afya. Katika Manispaa yetu ya Songea, kituo cha afya cha Mjimwema ambacho hivi karibuni kinatarajia kupandishwa hadhi na kuwa Hospitali ya Wilaya pana shida kwani hakuna vifaa vya upasuaji. Leo hii tunakwenda kupitisha hii bajeti ya TAMISEMI, labda Mheshimiwa Waziri ataniambia katika eneo hili kuna pesa ambazo zimetengwa? Nimejaribu kuangalia hapa sijaona na kama nilichokiona bado ni kidogo na ndiyo maana kama vile sijaona. Kwa hiyo, niombe katika kituo hiki cha afya ambacho kinakwenda kupandishwa hadhi mwezi wa saba basi kuwe na umuhimu kuhakikisha kwamba vifaa vya upasuaji katika chumba cha upasuaji vikamilishwe ili inapopanda kuwa Hospitali ya Wilaya iwe pia imetekelezwa kwa kiasi hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende pia kwenye eneo hilo hilo la afya katika Wilaya ya Mbinga. Katika Hospitali ya Wilaya kuna tatizo kubwa la mortuary ambayo haijapewa vifaa vinavyostahili ikiwemo fridge. Sifa ya mortuary ni kuwa na fridge na kama haina fridge basi hiyo sio mortuary. Kwa hiyo, niombe kupitia Waziri wa TAMISEMI afanye kila linalowezekana kuhakikisha kwamba katika Hospitali ya Wilaya ya Mbinga kunakuwa na vifaa ambavyo ni fridge na vifaa vingine ambavyo vinastahili katika mortuary hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende pia kwenye eneo la kilimo. Juzi nilisema hapa lakini pia naomba leo niseme labda nikisema sana itaeleweka. Kwenye eneo hili la kilimo katika mkoa wetu nimeshasema sana na nadhani hata Waziri wa Kilimo anafahamu kwamba Mkoa wetu wa Ruvuma ni mkoa ambao unazalisha mazao kwa wingi sana hasa mazao ya chakula. Kwa hiyo, ni vizuri mkoa huu ukapewa kipaumbele kwa kupatiwa pembejeo za kilimo kwa maana ya vocha zikawa nyingi zaidi ya zile ambazo zinapelekwa huko kwa sababu zilizopo bodi hazikidhi. Pia nipongeze mpango huu wa Serikali wa kuhakikisha kwamba unatoa pembejeo za kilimo kwa mpango wa vocha ili kuwawezesha wananchi kujikimu katika shughuli hizi za kilimo ili waweze kuzalisha zaidi. Chagamoto zilizopo ni pamoja na ufinyu huo wa pembejeo lakini pia ni pamoja na kuchelewa kwa pembejeo ambazo zinapelekwa kwenye maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hilo hilo kuna changamoto kubwa ambayo imekuwa ni kero sana, wakulima wanakwenda kulima na wanalima vizuri kwa kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa maana ya kilimo kwanza na wamekuwa wakizalisha sana. Shida inakuja wamepata pembejeo na wengine wanajiwezesha wenyewe kwa kununua pembejeo kwa bei ghali hatimaye sasa inafika mwisho wa siku anaporudisha mazao yake kutoka shambani ni tatizo kubwa, ushuru umekuwa ni kero. Kumekuwa na kero kubwa sana ambayo inasababisha hata watu wanaona shida kulima. Mtu analima labda kata fulani, anapotoa mazao kutoka kata hiyo kwenda kwenye kata nyingine katika Wilaya hiyo hiyo kunakuwa na barrier lukuki. Kwa mfano, katika Wilaya ya Namtumbo, ukitoka Mputa kwenda Hanga pana barrier, ukitoka Hanga kwenda Msindo pana barrier, ukitoka Msindo kwenda Lumecha pana barrier, hii ni kero. Pia kuna barrier kati ya Mwanamonga na Mwengemshindo, ni kata hizo hizo tu kunakuwa na barrier karibu 30 katika Wilaya moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali na Waziri wa TAMISEMI ajaribu kuona namna ya kuweka mikakati ya utafutaji wa pesa kuziwezesha halmashauri zake siyo kuwakamua wananchi. Kwa sababu unapokwenda kumkamua mwananchi ambaye amehenya miezi sita ili aweze kupata mazao halafu mwisho wa siku anakuja anakamuliwa kwa kukatwakatwa huu ushuru nalo si jambo jema. Ni sawaswa na mtu una mgonjwa unamuongezea damu huku upande mwingine unampachika mrija wa kumnyonya damu, hii haina mashiko na wala haina afya.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba ya Utumishi na Utawala Bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninapenda tu niishauri Serikali yangu kwamba suala la watumishi wa umma kwenye Wizara ya Afya na Elimu ni muhimu sana, kwa sababu tunapozungumzia maendeleo ni lazima tuhakikishe kwamba wananchi wetu wana afya njema. Kwa hiyo, watumishi wamepungua sana kwenye maeneo hayo kwa hiyo wapelekwe watumishi wa kutosha na kwamba tumesikia juzi kwamba kuna ajira mpya ya kwenda kwenye maeneo hayo. Basi ajira hizo zifanywe kwa wepesi kwenye maeneo hayo (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, demokrasia, tunazungumza suala la demokrasia katika nchi yetu, tunamshukuru Mungu sana nchi yetu imeendelea kuwa vizuri zaidi kwenye masuala ya demokrasia na ndio maana maendeleo yanazidi kupaa kwa kasi katika nchi yetu ya Tanzania. Niseme tu hapa mimi nitazungumzia kidogo kwenye suala la ukatili wa kijinsia. Kumekuwa na ukatili wa kijinsia hasa kwa Wabunge wa Viti Maalum wa vyama vyote tunapokuwa tunawajibika kwenye maeneo yetu kutekeleza wajibu wetu kama Wabunge wa Viti Maalum, tumekuwa tukinyanyapaliwa, tukinyanyaswa na Wabunge wenzetu wanaume kwa maana ya hofu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hasa pale ambapo Mbunge wa Viti Maalum anatoka Jimbo moja na Mbunge wa Jimbo hilo, wanakuwa na wasiwasi hofu yao ni kwamba Mbunge wa Viti Maalum akifanya kazi eneo hilo maana yake mwisho wa siku atapata mileage na kwamba anaweza akagombea Jimbo. Mimi niwaombe tu ndugu zetu Wabunge wenzetu kwamba sisi sote tunajenga nyumba moja mtupe nafasi tufanya kazi kwenye maeneo yote bila kutuwekea vipingamizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii unyanyapaa huu sasa hivi umekuwa ukiota mizizi, tumekuwa tukitishiwa, tunaambiwa maneno makali na hata wakati mwingine kutudhoofisha ili tusiweze kufanya kazi. Niombe sana Mheshimiwa Rais jana ametoa hotuba nzuri sana, kwa hiyo niseme tu kwamba tunamsubiri mama yetu akabidhiwe kijiti kwenye chama, sisi kama Wabunge wa Viti Maalum tunaopitia Chama cha Mapinduzi tutakwenda kwake ili atusaidie namna gani tuweze kufanya kazi ili kukomesha huu unyanyapaa kwa Wabunge Wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naenda kwenye masuala ya biashara. Juzi juzi; ni wiki tatu tu baada ya kifo cha aliyekuwa Rais wetu Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, tumesikia hotuba ya Mwenyekiti mmoja ambaye ana Mbunge mmoja wa chama chake ndani ya Bunge, lakini ana Wabunge 19 wa Viti Maalum akizungumzia kunyanyaswa na kufanyiwa vitu tofauti dhidi ya biashara zake. Sasa nataka Watanzania watege masikio ninataka niwaeleze ukweli juu ya masuala mazima yanayohusiana na Mheshimiwa Freeman Aikaeli Mbowe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninasema hivi kwa sababu ile ameizungumza hadharani na amehutubia katika …, kwanza inasikitisha sana muda mfupi tu baada ya Rais wetu kufariki badala ya kuja aeleze katika maelezo yake na masikitiko yake angeeleza hata baadhi ya kazi nzuri ambazo amezifanya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, badala yake ameeleza kinyume chake, lakini hatumshangai ni kwa sababu alikuwa anatetea tumbo lake. Niseme tu alieleza kwamba Serikali ilimfanyia ukatili wa kuzuia biashara zake na kuzifunga.

Mheshimiwa Spika, ukweli uko hivi, katika biashara yake yeye zile biashara anazozifanya ni za urithi wa kifamilia, na kwa kuwa ni za urithi wa kifamilia yeye amejimilikisha kama za kwake na kwamba hatoi mrejesho kwa ndugu zake, kwa hiyo ndugu zake wakaenda mahakamani, walivyokwenda mahakamani wakataka haki itendeke. Mahakama ikatoa amri ya kufunga biashara zake ili asiendelee na biashara mpaka mgogoro utakapokwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii anakuja anawadanganya Watanzania, anatafuta kuendelea kujipambanua kisiasa na wananchi wamwamini, hii si kweli na haikubaliki. Kwa hiyo, arudi akamalize mgogoro na familia yake asisingizie Serikali kwa imemnyanyasa na kumfungia biashara zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kuna jengo la Bilcanas lile jengo lilikuwa ni la Serikali la National Housing. Amekaa pale miaka na miaka halipi kodi anapenda vitu vya bure. Serikali ilipokuja kudai kodi analeta blaa blaa, Serikali iliyokuwa inaongozwa na Dkt. Magufuli ilikuwa haitaki blaa blaa na hata hii sasa inayoendeshwa na Mama yetu Samia Suluhu Hassan nayo haitaki blaa blaa. Asiyelipa kodi akae pembeni. Kwa misingi hiyo… (Makofi)

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani kuna Taarifa. Mheshimiwa Aida Khenani.

T A A R I F A

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa Taarifa mzungumzaji lakini pia niombe kiti chako kituongoze. Mimi ni Mbunge wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo - CHADEMA, kinachozunguzwa hapa ni Wizara ya Utumishi, kuzungumzia maisha ya mtu binafsi ndani ya Bunge ambaye hawezi kujibu, tena hazungumzii mambo ambayo yanayohusu mjadala uliopo anazungumza maisha yake binafsi, tuna Kanuni zetu niombe utaratibu wa kiti chako utuongoze. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Kwanza umesimama kwa Kanuni ya Taarifa, na Taarifa huwa anapewa mzungumzaji sio mwongozo wa kiti, lazima na wewe uwe umezitazama Kanuni vizuri. Na umesema vizuri hoja iliyopo mezani ni ya Utumishi na Utawala Bora, na Kanuni zetu zinaruhusu mtu ambaye alijadiliwa humu ndani kama anaona kile alichojadiliwa amevunjiwa heshima ama hakijawekwa kwa namna ambayo ni uhalisia, Kanuni zetu zinaruhusu namna yeye anavyoweza kuleta malalamiko. (Makofi)

Sasa Mheshimiwa aliyekuwa anachangia, mimi huwa nasikiliza hapa kila neno linalozungumzwa nasikiliza, Mheshimiwa anayechangia anasema huyu aliyetajwa alisema hoja hizo kuonesha nchi hii haina utawala bora na hoja iliyoko mezani inahusu utawala bora. (Makofi)

Kwa hiyo yupo sahihi kwa mchango wake, lakini kuhusu taarifa anazozisema kama kuna mtu humu ndani anafikiri anasema uongo asimame kwa kanuni inayosema kama Mbunge anazungumza uongo. Na kama yeye akisema uongo kuhusu huyo mtu Kanuni zetu zinaruhusu ataleta malalamiko yake kwa Mheshimiwa Spika utaratibu wa kawaida utachukuliwa kama huko nyuma ambavyo imewahi kutokea.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Msongozi.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana bado dakika zangu sita naendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapinzani wamekuwa wakiitupia sana Serikali malalamiko juu ya matumizi ya fedha za umma, ni jambo jema, lakini tunapozungumza usawa na kuangalia namna ya uwasilishaji wa mambo yenyewe ni vizuri sasa wewe mwenyewe unayewasilisha jambo hilo ukajitazama kwanza, wanasema tazama kibanzi cha jicho lako kabla hujamuonesha mwenzako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa misingi hiyo nataka niseme Chama cha Demokrasia na Maendeleo tunataka watueleze miaka mitano iliyopita fedha za ruzuku wamefanyia nini? Wamekuwa wakilipwa shilingi milioni 310 huyo Mwenyekiti huyo aseme shilingi milioni 310 kila mwezi, nimekokotoa vizuri nikapiga mara miezi 12 na mara miaka mitano nikakuta kwamba ni shilingi bilioni 18.6 ambazo chama hiki kimepelekewa pesa hiyo na kwamba katika utekelezaji wa majukumu yao dhidi ya ruzuku hii hawajajenga hata jengo moja ambalo lingewasaidia sasa kuonyesha taswira nzima ya chama chao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ikapelekea kwamba walishindwa kufanya uchaguzi kwa sababu hawakuwa na pesa, badala yake wakaja wakaanza kusema kwamba uchaguzi…

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …haukuwa wa haki haukuwa huru. Wewe ndugu yangu umekaa kwenye kiti tulia mambo yaendelee, wenzako wako nje huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme sasa…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani subiri kidogo.

Mheshimiwa Aida Khenani umeshatoa Taarifa kwa Mbunge huyu tayari wakati anachangia, labda usimame kwa Kanuni nyingine. Umeshatoa taarifa kwa Mbunge huyu anayechangia, Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, na Mheshimiwa Freeman Aikaeli Mbowe alipoona ameshafilisi kabisa chama chake akaamua kumsusua Tundu Lissu uchaguzi na kwamba sasa Tundu Lissu akawa anafanya peke yake, lakini ofisi hawana, lakini pia Mheshimiwa ….

Mheshimiwa Naibu Spika, bado dakika zangu tatu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa David Kihenzile anasema ameshamaliza kuongea, kwa hiyo huwezi kumpa Taarifa Mbunge ambaye ameshamaliza kuzungumza ahsante sana. Ahsante sana.

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Ameshamaliza?

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Aida Khenani hamna Mbunge anatoa taarifa zaidi ya mara moja kwa mtu mmoja, tafadhali. Mbunge unapotoa taarifa kwa Mbunge huwezi kuwa mnajibizana ninyi, ukishatoa taarifa umeshatoa mwambie jirani yako asimame ampe hiyo taarifa.

Waheshimiwa Wabunge tunaendelea. Umesema umemaliza Mheshimiwa ndiyo maana nimeikata ile taarifa nyingine kule ama nimesikia vibaya? Ulikuwa umemaliza au hapana?

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Alikuwa bado, bado hajamaliza Mheshimiwa.

NAIBU SPIKA: Waheshimwa Wabunge, tusikilizane nazungumza na Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani msimsaidie kujibu.

Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani nilizuia ile taarifa ya Mheshimiwa David Kihenzile nikifikiri umeshamaliza kuzungumza, si umeshasema unaunga mkono hoja. Mheshimiwa haya Mheshimiwa David Kihenzile.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ….

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa nilikuwa nataka kumpa Taarifa mzungumzaji kama viongozi wa chama fulani wametueleza mambo ya utawala bora kwa miaka mitano mfululizo na tumeshuhudia ndani ya chama kwa maelezo uliyotupatia. Nataka kumpa taarifa kuanzia sasa kwa kuwa pesa zimetumika zote hizo za ruzuku na hakuna chaguzi za ndani, wamekosa legitimacy na moral authority ya ku-question viongozi wa Serikali katika nchi hii kwamba hakuna utawala wa sheria. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge nadhani wote tunazo Taarifa za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali, ile taarifa ndiyo inayotuongoza kama huko kuna shida au hakuna shida. Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani malizia.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Kwa hiyo, Mheshimiwa yule mwenye Mbunge mmoja wa Jimbo Bungeni humu alienda kununua matrekta mawili, hayo matrekta mawili hayajulikani yaliko mpaka leo hii. Lakini amekuwa akizungumza kwenye maelezo yake kwamba kulikuwa na dhambi na ubatili mkubwa sana kwenye utawala wa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Mama Samia; hii si kweli kwa sababu hawa watu kama ndivyo ina maana kwamba ubatili wao ni kujenga zahanati 1,900? Ubatili wao ni kujenga hospitali 400 zaidi? Ubatili wao ni kujenga hospitali za mikoa 10? Ubatili wao ni kujenga flyover? Ubatili wao ni kununua ndege? Ubatili wao ni kujenga barabara? Haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Nbu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuipa fursa hii. Kwanza kabisa naomba niende kwenye suala la mifugo. Wakati ninakwenda kuchangia Bajeti hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania naomba moja kwa moja nianze na Wizara ya Mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia suala la ufugaji wa samaki kwa maana ya vizimba. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ametenga fedha shilingi bilioni 20 kwa ajili ya uwezeshaji kwenye eneo hilo la suala la ufugaji wa samaki kwenye vizimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tarehe 5 niliuliza swali linalohusisha ufugaji wa samaki hao na ikaonekana kwamba fedha hii imetengewa Shilingi bilioni hizo nilizozitaja na kwamba inakwenda kupelekwa kwenye Ziwa Victoria. Swali langu la pili la nyongeza nilikuwa nimeiomba Serikali kwamba ipeleke gawio sawa na maziwa mengine. Isiende shilingi bilioni 20 hii yote katika Ziwa Victoria bali iende na kwenye maziwa mengine ikiwemo Tanganyika, Ziwa Nyasa na Ziwa Rukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Waziri wa Mifugo Mheshimiwa Abdallah Ulega baada ya swali langu aliniita ofisini kwake na akaniambia ameshazungumza na timu yake sasa tunapata gawio, Ziwa Nyasa tunapata gawio la shilingi bilioni tatu ambayo itapelekwa kwenye suala la ufugaji wa vizimba katika Ziwa Nyasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine naomba niende kwenye suala la viwanda na biashara. Kwenye suala la viwanda na biashara naomba niende moja kwa moja katika Kata ya Mwengemshindo katika Manispaa ya Songea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, EPZ walichukua maeneo ya Kata hiyo ya Mwengemshindo ni miaka 15 sasa tangu maeneo hayo yamechukuliwa na wananchi bado wanalia hawajalipwa fidia, hawaelewi hatma ya maisha yao. Wanashindwa kuendeleza aidha kuongeza kama ujenzi wa nyumba au kufanya shughuli nyingine zozote zile za maendeleo. Fedha hii Shilingi bilioni 3.9 leo hii nimesimama hapa katika Bunge lako tukufu ninataka Mheshimiwa Waziri Mkuu atakapokuja ku-windup hapa aniambie ni lini Serikali itapeleka fedha hii shilingi bilioni 3.9 kwa wananchi wa Kata ya Mwengemshindo katika Manispaa ya Songea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende kwenye miundombinu, naomba nizungumzie barabara ya kilometa 28 ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais. Barabara hii inatoka Mbinga mjini inapita katika Kata ya Ruwaita, inapita Kindimba, Mahenge, Litembo ambayo barabara hii ni barabara ya kimkakati. Mheshimiwa Rais alikuja pale na akatoa ahadi, Rais wa Awamu ya Sita akiwa Makamu wa Rais alitoa ahadi pale kwamba barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Sasa ni wakati muafaka, ninaomba fedha hii itengwe ili barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika naomba niende kwenye barabara ya kilometa 35 ambayo inatoka Kigonsera kwenda Matili yenye urefu kilometa 35 ambayo inapita Kitumbalomo, Lukalasi. Matili ni kata ambayo ndiyo inabeba uzalishaji mkubwa wa mazao ya nafaka katika Mkoa wetu wa Ruvuma. Kwa hiyo, ninaomba barabara hii sasa ni wakati muafaka fedha ipelekwe ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami na Mheshimiwa Benaya Kapinga amekuwa akizungumzia sana barabara hii. Naomba sasa kwa heshima hiyo ya Mheshimiwa Kapinga na mimi Jacqueline Ngonyani Msongozi, barabara hii sasa iweze kutengewa fedha na iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye Barabara ya Likulufusi – Mkenda yenye urefu wa kilometa 124. Hii ni barabara ambayo inaunganisha Nchi yetu ya Tanzania na Nchi ya Mozambique na barabara hii nimekuwa nikiimba kila nikiamka kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka husika lazima niisemee barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama ambaye ndiye inapita kwenye jimbo lake amekuwa akiizungumzia sana hii barabara na sasa mimi pamoja na yeye kwa heshima hiyo tunaomba barabara hii ianze kujengwa haraka sana kwa sababu barabara hii ni barabara ambayo itaunganisha hizi nchi mbili. Manufaa ya barabara hii ni kwamba itasaidia kuchochea uchumi katika Nchi yetu ya Tanzania, itasaidia kuimarisha soko ambalo limjengwa kwenye Mpaka wa Tanzania na Mozambique pale Mkenda. Tuna soko ambalo limejengwa mpaka sasa fedha ya Serikali imetumika lakini bado halitumiki kwa sababu miundombinu ya barabara pande zote mbili haijakaa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii itaongeza biashara kwenye eneo hilo la mpaka. Itaongeza mzunguko wa fedha katika Manispaa ya Songea na Jimbo la Songea Vijijini, Jimbo la Peramiho kama nilivyosema. Pia wananchi wa kutoka Mozambique watatumia uwanja ule wa ndege wa Songea ili kuweza kusafiri kwenda kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa barabara hii itatengewa fedha kwa maana ya heshima hiyo lakini pia mumpe heshima Chief Whip wetu ambaye amekuwa akifanya kazi hapo wakati mwingine anakosa fursa ya kusema kama ninavyosema basi mpeni hiyo fursa ya hiyo barabara ni barabara muhimu sana ili tuweze kufikia malengo tunayokusudia kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ukarabati wa shule kongwe. Iko Shule ya Sekondari ya Msindo iliyopo katika Wilaya ya Namtumbo katika Mkoa wa Ruvuma. Hii shule ni kongwe, shule hii imechakaa sana inahitaji ukarabati, halikadhalika katika shule hiyo hiyo kunahitajika hostel ya watoto wa kiume. Kimsingi wamekuwa wakilala kwenye jengo ambalo halifai na wala jengo hilo ni kama vile ghala. Kwa hiyo, tunaomba Serikali ifanye jitihada za makusudi ili kuokoa ustawi wa watoto wale mwisho wa siku tunahisi kwamba wanaweza wakapata magonjwa mengine kwa sababu jengo hilo wanalokaa vidirisha ni vidogo sana kwa sababu ni ghala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika sekondari hiyo hiyo kuna hitaji la bwalo la chakula la shule hiyo. Sasa hivi wanapikia kwenye eneo la wazi, kwenye mti nje wanapikia chakula hapo. Kwa hiyo, ninaamini bwalo likishajengwa maana yake hata ustawi wa afya zao wale watoto wetu zitakuwa ni njema. Kwa hiyo, niiombe Serikali ifanye hivyo haraka sana ili kuokoa hali halisi na mazingira halisi yanayojitokeza kwenye shule hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la afya, Wananchi wa Kata ya Msindo wamejenga jengo la upasuaji katika eneo la jengo ambalo lilianza awali kabla ya kituo cha afya hakijajengwa. Jengo lile wananchi wamejitolea wamefikia kiwango cha kuezeka lakini hawawezi kuendeleza kwa sababu hawana fedha ndiyo wameishia hapo. Tunaomba msaada wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ipelekwe fedha pale ili waweze kwenda kumalizia jengo lile la upasuaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka sasa niendelee kwenye suala hilo hilo la afya. Tarafa ya Mbuji katika Wilaya ya Mbinga, Jimbo la Mbinga Vijijini ni tarafa ambayo inabebwa na Kijiji cha Mpaka, Unyoni, Litembo, Mbuji, Kitulo. Tarafa hii yenye vijiji hivyo vikubwa bado haina kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Mheshimiwa Waziri Mkuu wewe unafahamu vizuri Mkoa wa Ruvuma, tunaomba sasa upeleke kituo cha afya kikajengwe kwa ajili ya kuokoa maisha ya wananchi ambao wanaizunguka tarafa ile, kwa maana ya kata tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu zahanati. Katika jimbo hilo hilo, wilaya hiyo hiyo ya Mbinga bado kuna tatizo la zahanati, zahanati hakuna. Nilipokuwa nazungumzia kituo cha afya maana yake hata zahanati huko chini hakuna. Kuna uhitaji wa zahanati 38 katika eneo hilo. Mheshimiwa Banaya amekuwa akipiga kelele hapa kila siku anaomba zahanati zijengwe katika maeneo haya. Sasa na mimi kama mama nimesimama hapa katika Bunge lako kulisemea hilo hilo. Nipaze sauti, labda kwa sababu ni mama, ili wananchi hawa waweze kupata fursa ya kujengewa zahanati na nitataja baadhi siwezi kutaja maeneo yote 38; basi nitataja baadhi itakuwa ni wakilishi kwa maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zahanati hizo zinazotakiwa zijengwe ni katika Kijiji cha Likoho, Lugavi, Njombe, Kizota, Ukata, Lisao, Mzuzu, Mhagawa, Mtaya, Liyombo, Liuhula na nyinginezo. Naomba maeneo haya yatengewe fedha ili zianze kujenga. Safari ni hatua, hata ukitutengea 10 tu itakuwa ni hatua nzuri kwa mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka niliongelee ni suala la mmomonyoko wa maadili…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jacqueline nakuongezea dakika moja tu malizia hilo kwa sababu ni la maadili.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwenye suala la mmomonyoko wa maadili naomba tu niseme kwamba tuna kila sababu sisi kama Wabunge kuhakikisha kwamba tunaleta sheria iwe ya mkazo hapa Bungeni, itengenezwe sheria na sisi tuipitishe kama Bunge ili kuweka utaratibu mzuri ambao utawafanya wale wanaoshughulika na mambo haya waweze kubanwa kwa namna moja au nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa kwa kuwa wewe ulikuwa Makamu Mwenyekiti naomba upendeleo wa dakika moja. Naomba nitumie nafasi hii kuwapongeza sana viongozi wa dini ambao wamejitokeza kuzungumzia suala la mmomonyoko wa maadili katika nchi yetu. Tumeona Shehe Mkuu wa Tanzania amesema, tumeona maandamano kule Arusha, na tumeona viongozi wa madhehebu mbalimbali wanazungumza sana kuhusiana na kukemea kuhusu jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona pia viongozi hawa wa dini wa madhehebu mbalimbali wote ambao wanakemea, lakini nampongeza sana Apostle Buludoza Boniphace Godwin Mwamposa. Yeye kabla ya kuanza ibada kila jumapili anaanza kukemea jambo hilo na wote wafanye hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Jacqueline.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri mwenye dhamana…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Jacqueline…

MHE. HACQUELINE N. MSONGOZI:… wa maendeleo na ustawi wa jamii hatujamsikia sauti yake akikemea jambo hili hatumwelewi tunaomba atoke na aseme kuhusu jambo hili.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ili namimi niweze kuchangia kwenye hii Bajeti ya Wizara ya Maliasili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wangu kipenzi Dtk. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri sana aliyoifanya kupitia suala la Royal Tour, kiasi ambacho sasa imetoa taswira nyingine kabisa katika nchi yetu ya Tanzania kwenye masuala ya utalii. Nampongeza sana mama yetu huyu kwa sababu amekuwa akijitoa, ni mzalendo wa nchi yetu hii ya Tanzania. Hata nyinyi wenyewe pia Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi nchi imetulia kila kitu kinaenda sawa, uchumi unaendelea kukua, miradi yote inaendelea kutekelezwa, mikubwa na midogo yote inakwenda barabara, heko nyingi sana kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana Waziri mwenye dhamana ya utalii ambaye ni kaka yangu Mohamed Mchengerwa lakini pia na delegation yake yote kwa namna ambavyo wanachapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende kwenye matukio ya tembo kuuwa na kujeruhi katika Wilaya ya Tunduru kwa kipindi cha mwaka 2020 mpaka kufikia sasa 2023. Kwa masikitiko makubwa sana naomba niseme kwamba tembo tunawapenda sana, ni rasilimali ya Taifa na wamezaana sana na ni kivutio kikubwa sana kwa watalii. Lakini mimi najiuliza tu, hivi ili mtalii aje amtambue tembo inabidi tembo hao wawe wanasindikizwa na sifa ya maelfu ya tembo wangapi? Kwa sababu tembo hawa wamekithiri wanafika mpaka kwenye makazi ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu kama ni shambani ukiweka viazi kwenye nyumba wanapenda ile harufu ya viazi wanakuja wanabomoa mpaka nyumba wanachukua viazi wanaenda kuvitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nataka niseme hivi, natoa wazo sasa kwamba ni kwanini Mheshimiwa Waziri hawa tembo tusifikirie kuwavuna baadhi? tunawavuna wapungue kidogo kwa sababu bado wana kizazi waendelee kuzaa. Wale wanaopungua sasa maana yake ni nini, tutaenda kutoa yale meno tutayaweka kwenye Benki yetu ya Taifa ya Rasilimali za Taifa lakini pia nyama zile tutaweza kuuza kwenye mabucha yetu kwa sababu wako watu ambao wanakula. Kwa hiyo hii ni mali kwa mali. Tukiwavuna hadha pia itapungua. Wakati wanaendelea kuzaa basi wanachi wapate hafuweni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema kwamba mwaka 2020 katika Wilaya ya Tunduru pamoja na Namtumbo pia watu tisa walikufa na watatu kujeruhiwa; 2021 kufa watu wawili na saba kujeruhiwa, 2022 kufa watu nane na sita kujeruhiwa, 2023 kufa watu sita na sita kujeruhiwa katika Wilaya ya Tunduru tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya watu ambao wamekufa katika Wilaya ya Tunduru tangu mwaka 2020 mpaka 2023 walikuwa ni watu 25 na waliyojeruhiwa ni watu kumi saba, ni watu wengi sana, rasilimali ya nchi hii inapotea. Hata hivyo endapo kama wanapata majeraha na kufa bado inaonekana kwamba mnyama anathamani zaidi kuliko binadamu. Sasa hebu tuondoke kwenye hiyo adha. Kama kuna kanuni au sheria inatakiwa irekebishwe kwa mustakabali huo kwa maana yaku-balance binadamu na wanyama basi mimi nataka niseme hivi sheria hiyo iletwe hapa Bungeni ili tuirekebishe. Na kimsingi hauwezi kulinganisha mnyama na binadamu hasilani abadani haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka niseme kwamba fidia inayotolewa kwa mwananchi akiuwa ni shilingi laki moja tofauti na thamani ya binadamu lakini pia mwananchi aendapo kama ataliwa mazao yake fidia anayopewa ni shilingi laki mbili, laki moja mpaka laki tano. Mwisho huyo anakuwa amefilisika kabisa na wameona kwamba hili shamba ni kubwa wanaona aibu hata kumwambia kwamba haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende kwenye migogoro ya vijiji ambavyo vinazungukwa na wanyamapori. Nimpongeze Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kushughulikia migogoro hii. Kwamba sasa hivi punde nimesikia kuna taasisi au nchi imetoa fedha takriban bilioni 149 hivi kwa jili ya kusaidia mikoa ambayo inakutana na changamoto hiyo ya kuvamiwa na kushughulikiwa na wanyamapori. Kwa hiyo changamoto za wakulima na hifadhi za wanyamapori imekuwa ni kubwa kiasi ambacho sasa ameona kwamba atafute fedha kwa ajili ya kwenda kushughulikia changamoto hizo. Pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais, na niombe Wizara ifanye vizuri sana kwa ajili ya kumpa sapoti Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende kwenye suala ambalo kimsingi nataka niliseme, linahusiana na suala la kauli, lugha mbaya kwa wananchi. Kabla sijalisema hilo naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Mchengerwa, Mheshimiwa Mchengerwa anafanya kazi nzuri sana. Tunamsemea hapa vizuri kwa sababu you deserve the best, unafanya vizuri kabisa si, kwamba unapendelewa, sifa hiyo unastahili. Kwakweli unafanyakazi nzuri; na wengine wamesema ulitoka kwenye michezo, ulitoka kwenye utumishi kote huko umefanya vizuri umeacha alama. Sasa hivi uko maliasili na utalii tunategemea kwamba Wizara hii sasa inakwenda kuchanja mbuga na kuleta matokeo chanya katika nchi yetu hii ya Tanzania. Hongera sana nikutie moyo, endelea kufanya kazi na sisi kama kuna jambo lolote la kukusaidia ndani ya Bunge hili lilete tukusaidie, tuchakate ili kazi iweze kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza pia kwa namna ambavyo amekuwa akitatua migogoro anatatua migogoro kidiplomasia, anakwenda site anazungumza na wananchi. Mwananchi hata kama alikuwa ana-burden gani anajikuta kabisa anacheka, anafurahi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikia Mheshimiwa Mchengerwa akiwa Wilaya ya Mbarali ambako kulitokea changamoto, ameondoka kule wananchi wanafuraha sana; endelea kufanya hivyo Mheshimiwa Mchengerwa. Lakini pia nimesikia amekwenda kule Tarime Vijijini, nako amefanya vizuri, tumeoa clip zake na ambavyo anaongea na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu Mchengerwa anafahamu kwamba ili sisi tukae humu ndani ya jumba hili ni lazima wananchi wapige kura kumchagua Mheshimiwa Rais, kuwachagua Wabunge, kuwachagua Madiwani na hata Wenyeviti wa Vitongoji anafanyakazi nzuri. Lakini wako wengine wanasahau kwamba ili kukaa humu ndani basi hakuna haja ya kutambua hivyo vitu. Ni muda mfupi sana jamani, tusisahau, na ni muda mfupi sana wa kukaa humu baadaye tunatoka kwenda kuomba kura kule. Sasa kama hatutambui umuhimu wa wale wananchi maana yake mwisho wa siku tutakwenda kule na tutarushiwa mawe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme jambo moja kwa masikitiko makubwa sana. Leo hii niseme kwamba nilikuwa nategemea Wizara hii inapokuja na bajeti yake basi Naibu Waziri wa Maliasili awe alishakwenda kule Tarime Vijijini ameomba msamaha kwa wale wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imetembea clip yake nchi nzima ambayo ilikuwa na maneno, ambayo siyo mazuri, siyo maneno ya kiungwana, maneno ambayo kiukweli hayana mahusiano mazuri na wananchi yanachonganisha baina ya Serikali na wananchi, ni maneno ya udhalilishaji kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka niseme ni maneno ya udhalilishaji kwa wananchi. Huwezi kwenda kuwaambia wananchi eti kwamba mnageuza huko porini ni sehemu ya kwenda kujisaidia, hapana siyo sawa. Kwa sababu hawa wananchi maana yake ni nini? Hawajui suala la usafi, hawana vyoo, hawajawahi kujenga vyoo. Naomba kupitia Bunge lako Tukufu huyu Mheshimiwa Naibu Waziri aende kuomba msamaha, sisi kama wananwake wenzake tunaksikia aibu kuongea maneno ya udhalilishaji kama yale kwa wananchi wale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana aende akaombe msamaha kwa wananchi wale ambao alitumia kauli mbaya kuwajibu, wale ni wananchi wa Tanzania. Tunawategemea kwa kazi alizofanya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, anastahili apewe kura zote 100% badala…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Msongozi muda wako umekwisha.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, umesahau, kwa hiyo naomba sekunde moja tu. Kwa hiyo sasa nataka mimi nitashika shilingi kwenye eneo hili endapo kama Naibu Waziri hataomba msamaha hapa wakati tuna - wind up, aombe msamaha kwa wananchi wale kwa kile ambacho aliwatendea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyenijalia kupata uzima siku hii ya leo, nikushukuru pia wewe mwenyewe kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Bajeti Kuu ya Serikali 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza na suala la ujenzi wa zahanati, vituo vya afya pamoja na hospitali ni jambo ambalo lilikuwa limelenga kabisa maendeleo yetu ili yaweze kufanikiwa ni lazima kwanza wananchi wetu wawe na afya bora na hapo ndipo tutakapoweza kufikia uchumi wa kati, lakini pia katika kufanikisha malengo ya milenia kufikia uchumi huu wa kati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niiulize Serikali leo ni lini itakamilisha ujenzi wa vituo vya afya, zahanati pamoja na hospitali za Wilaya ili tuweze kufikia sasa uchumi huu wa kati, kwa sababu tusipokuwa na afya njema ni wazi kabisa Taifa litakuwa na wananchi ambao ni goigoi, watashindwa kufanya kazi vizuri ili kuweza kufikia uchumi huu. Hivyo, Serikali iniambie lini ujenzi huu utakamilishwa katika vituo vile vya afya, zahanati pamoja na hospitali za Wilaya ambazo hazijawa tayari kwa maana ya kutumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kuainisha hizo zahanati ambazo zipo katika Wilaya ya Mbinga, Mbinga Mjini kuna zahanati karibu 15 ambazo zinahitaji kumaliziwa, lakini pia Mbinga Vijijini kuna vituo vya afya na zahanati ikiwemo katika Kata ya Kilimani kuna zahanati, Lipilipili, Luwahita, Luhaga, Mikatani na Kihuka. Pia katika Wilaya ya Nyasa pana shida kubwa sana kwa maana ya hospitali ya Wilaya imeanza na haijakamilika, ni lini Serikali itakamilisha ili tuweze kupata wananchi ambao watakuwa na afya bora tuweze kufikia malengo ya milenia.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya hiyo hiyo ya Nyasa kuna zahanati ya Chiwanda, Ngindo, Liweta, Mpotopoto, naomba pia nazo zitiliwe uzito zitengewe pesa kwa ajili ya kukamilisha. Tunduru pia kwenye eneo hili kuna wodi ya wanaume katika hospitali ya Wilaya ya Tunduru, watoto wa kiume wanaenda kulala kwenye wodi ya akina mama, hii ni hatari sana kiafya lakini pia hata kimaadili. Wodi ya wanaume kule Tunduru inatakiwa imaliziwe, lakini pia kuna wodi ya wanawake nayo pia imaliziwe katika Wilaya ya Tunduru nikienda sambamba na zahanati za Masonya, Sisi kwa Sisi, Cheleweni, Njenga na Fundimbanga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Madaba pia naomba mfahamu mchango mzuri wa Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Madaba na jitihada ambazo anaendelea kuzifanya ili kuhakikisha kwamba, Jimbo la Madaba litakuwa na hospitali ya Wilaya lakini pia na vituo vya afya pamoja na zahanati ili nao pia waingia katika malengo ya milenia. Hali kadhalika na katika Wilaya ya Namtumbo zahanati na vituo vya afya ni muhimu. Zahanati na vituo vya afya vikikamilika ni wazi kabisa tutakuwa tuko vizuri na afya zitaboresheka na hata hivyo tutafikia hizo asilimia saba za uchumi wa Tanzania ambao tunautarajia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kuondoa tozo zisizokuwa na tija kwenye mazao ya korosho, kahawa na tumbaku, naipongeza sana Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma bajeti hii na maelezo ya Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii kwa maana ya bajeti ya Serikali maelezo ni matamu na hata uchambuzi wake ni mzuri mno. Hii inaonyesha wazi ni namna gani Serikali imejipanga vizuri kuhakikisha kwamba inakuza uchumi wa ndani kwa kukusanya mapato pia inafikia hatua ambayo Serikali sasa itaacha kuwa tegemezi na itaenda kujitegemea yenyewe. Naipongeza sana Wizara hii kwa kujipanga vizuri kwenye eneo hili. Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake mko vizuri pamoja na delegation yote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia kwenye eneo hili iangalie sekta zile ambazo zimekuwa zikitoa mchango mkubwa sana kwa maana ya kuingiza mapato mengi katika nchi yetu ikiwemo sekta ya utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sekta ya utalii kumekuwa na jambo moja ambalo lilikuwa kama vile wenzetu ambao walikaa kwa maana ya mahusiano haya ya East Africa wakakaa kwa pamoja Mawaziri wa Fedha wakiwa na lile jambo ambalo kwa mfano, labda wanasema kwamba, kuna chakula cha mgeni na chakula cha wote. Kilichofanyika hapa ni kama hivi changa la macho.
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wa Kenya mara ya kwanza walikuwa wameingia kwenye suala la kutoza VAT kwa watalii wanaoelekea Kenya. Baada ya hapo wakaona kwamba ile VAT haitawasaidia na kwamba imeshusha sana kiasi cha mapato yanayopatikana katika utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 Mawaziri hawa walipokaa walikubaliana vizuri kilichojitokeza ni kwamba, mwaka 2015 Kenya ilipata watalii 3,000,000 na waliingiza dola za Kimarekani bilioni 1.5. Tanzania iliingiza watalii milioni 1,100,000 ilipata dola za Kimarekani bilioni 2.5. Sababu kuu ilikuwa ni kwamba Tanzania ililenga kuwa na watalii wakubwa tu ambao wana uwezo wa kulipia hoteli, lakini Kenya walikuwa wamelenga wapate watalii wadogo wadogo pamoja na kutoza kodi kwa hiyo mapato yao yalishuka. Baada ya kugundua hilo sasa wamerudi na habari nyingine wakasema kwamba, wao ni vizuri wakaondoa kodi kwa hiyo, tumebaki sisi ambao kimsingi tumeenda kujiingiza kitanzi wenyewe, tunaenda kujikaba wenyewe ili tujinyonge na hatimaye tushindwe kuongeza mapato kwenye eneo hili la utalii. (Makofi)
Waheshimiwa Wabunge wenzangu, niwaombe sana kwenye jambo hili tushirikiane, tufike mahali tukubaliane kama wamoja tuondoe VAT kwenye eneo hili la utalii ili utalii uendelee kuingizia mapato Serikali, kinyume na hivyo maana yake tutakosa hizi dola za Kimarekani bilioni mbili na point zake, badala yake wenzetu Kenya wanaenda kufanikiwa sisi tunabaki tuko tunabembea tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Wabunge kama nilivyosema nisingependa kurudia pia nitakuwa sijatenda haki endapo kama sitaongelea kodi ya Wabunge. Kwenye suala hili kwa kweli mmegusa pabaya, panaumiza kweli kweli ukizingatia kwamba Mbunge hata sasa mshahara wake bado anatozwa kodi kila mwezi Mbunge anakatwa shilingi milioni moja na laki tatu na kadhalika mpaka itakapofika miaka mitano maana yake kunakaribia milioni 50 ambayo Mbunge anakatwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba niwaambieni mimi kama Mbunge toka asubuhi mpaka sasa hivi hapa niliposimama nina simu 30 zinatoka kwenye Jimbo langu la Mkoa wa Ruvuma, wananchi wana mahitaji mbalimbali na ukizingatia kwamba Wabunge wa Viti Maalum hatuna Mfuko wa Jimbo, tunafanyaje kwa kile tunachokipata? Kile tunachokipata kidogo ndiyo kinaenda kusaidia hata ukaenda kufanya hili, ukafanya lile na hata kuwezesha vikundi mbalimbali. Ninaomba Waziri atakapokuja tena, aje na maelezo mazuri kuhusu eneo hili ili tuweze kwenda sambamba, vinginevyo hatumuelewi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana naomba kuunga mkono hoja.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi kukushuru kwanza kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia Kamati ya Huduma ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, pamoja na Ardhi, Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kupongeza uchaguzi uliopita tarehe 22 Januari, 2017 ambapo Chama cha Mapinduzi kiliwafunga wapinzani wetu wana UKAWA goli 22 kwa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana unajua tunajuana humu ndani wapo wanaokula msuba asubuhi, mchana na jioni kwa hiyo hainipi shida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niende kwenye suala la kilimo kwa maana ya ubora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba hiyo kazi wanayoifanya ndiyo iliyowaleta humu ndani na hawana kazi nyingine kama wangekuwa na kazi wangekuwa watulivu wasikilize nini kinachochangiwa sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ya Kilimo wawe makini sana kwenye suala la ubora wa mbegu. Mbegu zinazopelekwa kwa wakulima siyo mbegu sahihi, wakati mwingine mbegu zile huwa zinakuwa zina shida, hata kama ni mbegu ambazo zinatolewa kwa mtindo wa ruzuku lakini bado hazimsaidii mwananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisema kwamba kunai le hali ya mimba za utotoni, kwenye mbegu hizi nyingine nazo ni staili ya mimba za utotoni. Kuhusu hizi mbegu unakuta wakati mwingine mbegu zinakuwa ni fupi haziwezi kuzalisha kadiri ambavyo inastahili, kwa hiyo Wizara ya Kilimo tunaomba muwe makini. Pia niseme endapo mbegu hizo zisizokuwa na ubora zinaletwa, mwisho wa siku mwananchi anapokuwa amepata hasara, hasara hii inafidiwa na nani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee suala la mawakala wa pembejeo. Mawakala wa pembejeo hili ni jambo ambalo tumekuwa tukiliimba kila siku. Mawakala wa pembejeo ambao kimsingi waliikopesha Serikali, walifanya kazi ya kusambaza mbolea na mbegu mbalimbali kwa ajili ya kuikopesha Serikali mwisho wa siku mawakala hawa mpaka leo hawajalipwa. Toka mwaka 2014, mwaka 2015, mwaka 2016, ni lini Serikali hii itawalipa hawa mawakala? Wamekuwa na shida na wengine mpaka sasahivi wameshapoteza maisha na wengine wanadaiwa na mabenki, walikuwa wazima wakati wanakopesha mbolea hizi kwa wananchi, sasa hivi unakuta tayari wameshanunua magonjwa kama pressure. Naiomba Serikali iwe serious ili kuwasaidia hawa wananchi wajasiriamali ambao waliweza kuikopesha Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende pia kwenye Benki ya Kilimo. Wakati tunapitisha bajeti hapa mwaka jana mwezi wa sita, bajeti ya kilimo, Waziri alikuwa amesema kwamba angeweza kufikisha Benki ya Kilimo katika Mkoa wetu wa Ruvuma, lakini nashangaa mpaka sasa hivi bado haijafika, sijui ndiyo bado upembuzi yakinifu au ni nini? Mpaka sasa hivi hakuna dalili zozote zile za kufikisha benki hii ya kilimo! Niombe Waziri wa Kilimo tafadhali kwa kuwa mkoa wa Ruvuma ni mkoa ambao wananchi wake wanashugulika na kilimo kwa asilimia 92, naomba sasa benki hii iende ili iweze kuwasaidia wananchi hawa waweze kukopa na kuweza kufanya uzalishaji wenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la uvuvi; tunalo Ziwa Nyasa katika Mkoa wetu wa Ruvuma. Mimi naomba nishauri jambo hapa, uvuvi katika Ziwa Nyasa samaki walioko pale wangeweza kuwa wengi zaidi na uvuvi ule ukawa na tija endapo kama Serikali ingeweza kufanya kama wanavyofanya wenzetu wa Malawi, kwa sababu ziwa hilo moja liko upande Malawi na upande mwingine wa ziwa upo upande wa Wilaya ya Nyasa kwa maana ya Tanzania. Kwa hiyo, wenzetu wa Malawi wanachokifanya wanalisha chakula kwenye lile ziwa, samaki wanakwenda kwenye upande wa Malawi kwa sababu kuna chakula. Wenzetu wa Malawi sasa wanapata mavuno mengi kutokana na hili Ziwa Nyasa. Sisi tunaambulia patupu, ziwa lipo tunaambulia kuangalia tu mandhari ya ziwa lilivyo lakini hatuna faida nalo yoyote ile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali ione umuhimu kama tuko serious na suala hili la uvuvi, basi walao tufanye huo utaratibu wa kuwa tunalisha chakula ili tuweze kupata samaki wazuri ambao tutawauza na watatupatia pato…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante Jacqueline.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kupongeza Kamati ya UKIMWI kwa utekelezaji mzuri wa majukumu yao. Ushauri, jitihada za kupambana na kudhibiti madawa ya kulevya haziridhishi, kwa kuwa bado vijana wengi mitaani wanaendelea kuathirika. Ushauri kwa kuwa madawa ya kulevya yamekuwa na athari kubwa kwa jamii na Taifa kwa ujumla ikiwa pamoja na kupunguza nguvu kazi ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri Serikali iwe na mpango mahususi wa kufanya vipimo kwa vijana au watoto wetu mashuleni na mitaani wamekuwa na tabia ya kulawitiana . Kwa hiyo upimaji utasaidia kubaini na kudhibiti hiyo michezo hatarishi kwa watoto wetu. Aidha, nashauri upimaji huo uletwe pia hapa Bungeni ili kubaini waathirika wa ulawiti.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia taarifa hii ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii na Kamati ya UKIMWI. Namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa uhai ili niweze kusimama hapa siku hii ya leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la elimu bure. Nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kuthubutu kuweza kutekeleza elimu hii bure. Dhamira ni njema, lakini katika mpango huu bado kumekuwa na changamoto nyingi mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la elimu napenda kuzungumzia kwamba elimu bure sawa inatolewa, lakini pia ukienda kwenye shule zetu za primary na za secondary kumekuwa na changamoto ya upungufu wa madarasa; lakini bado katika Mkoa wangu wa Ruvuma kuna changamoto katika Wilaya ya Namtumbo katika sekondari ya Nungu Kata ya Hanga.
Kwenye hiyo sekondari ambayo sasa imeanza kidato cha tano; na changamoto iliyoko hapo inafanana kabisa na changamoto iliyoko katika Wilaya hiyo hiyo katika sekondari ya Nasulu Wilayani Namtumbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu sekondari hizi zilipoanzishwa kwa kidato cha tano hawajapelekewa pesa kwa ajili ya chakula. Kwa hiyo niombe, tunapoamua kutoa elimu bure ni vizuri basi tukajikita kwenye mambo ya msingi. Kwa mfano; mtoto hawezi kuendelea kusoma na akajituma vizuri zaidi na kuweza kuwa msikivu katika masomo kama hatakuwa amepata chakula. Wazabuni ambao wamejitokeza kutoa huduma katika shule hizi wameshafanya kwa kiasi walichoweza, lakini imefika mahali wanakwama kwa sababu hawajawezeshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa Walimu pia unachangia kwa kiasi kikubwa. Hili ni eneo ambalo wajumbe wenzangu wengine Waheshimiwa Wabunge wamechangia; kwamba bado maboresho dhidi ya Walimu hawa yanatakiwa ili Walimu waweze kuwa na moyo wa kuendelea kutoa huduma hii ya elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende pia kwenye suala la afya katika Wilaya hiyo hiyo ya Namtumbo. Hospitali hiyo inajengwa kwa takribani miaka mitano sasa na haijakwisha. Mpaka sasa hivi ninavyozungumza, hospitali hii ya Wilaya ya Namtumbo bado ina jengo la OPD tu, hakuna wodi wala hakuna theatre.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Wilaya ya Namtumbo ni wilaya kubwa sana na imejumuisha kata nyingi, zaidi ya kata 23, bado wilaya hii inahudumia pia mji mdogo wa Lusewa; Wizara ingefanya jitihada za makusudi kuhakikisha kwamba hospitali hii ya Wilaya inakwisha ili iweze kuendelea kutoa huduma kwa sababu akinamama wengi wajawazito wanapata shida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hizi kata zilizopo pale katika Wilaya ya Namtumbo nyingi zimekuwa kwenye maeneo ya mbali. Unakuta kutoka kwenye kituo au Makao Makuu ya Wilaya kwenda kwenye maeneo ya pembezoni, maeneo mengine yanafikia kama kilometa 100, kilometa 70 na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri kwenye Wilaya hii ya Namtumbo, kwa maana ya Hospitali ya Wilaya, angalau ingekamilishwa wodi ya akinamama ili kuweza kuwafanya akinamama waweze kujifungua salama. Kwa mfano; kuna kituo hiki cha Lusewa; Kituo hiki cha afya cha Lusewa kimekuwa kikihudumia wanawake ambao wakati mwingine wakizidiwa wanajikuta wanalazimika kwenda katika hospitali ya Mbesa ambayo iko karibu kilometa 150 kutoka Wilayani Namtumbo na usafirishaji wa akinamama hawa wakishakuwa kwenye hali mbaya mara nyingi wamekuwa wakibebwa na pikipiki. Yanatengenezwa matenga huku nyuma, wanawekwa kwenye matenga ili waweze kusafirishwa ili kufikishwa kwenye hospitali ya Mbesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, mama yangu Ummy, naomba asikie kilio hiki cha wanawake wa Mkoa wa Ruvuma ili waweze kusaidiwa kwenye eneo hili ambalo imekuwa ni eneo tete sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende pia kwenye Wilaya ya Tunduru katika zahanati ya Legezamwendo. Zahanati ya Legezamwendo ni zahanati ambayo imezungukwa na vijiji karibu sita; zahanati hii bado haijakamilika na sasa hivi tayari inakaribia miaka minne. Niombe basi zifanyike jitihada za makusudi kuhakikisha kwamba fedha zinakwenda ili zimalizie zahanati ile ili iweze kutoa huduma kwa wananchi ambao kimsingi baadhi yao tayari wameshapewa hata zile kadi za CHF ili waweze kuzifanyia kazi hizo kadi zao na waweze kupata huduma ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika katika Hospitali ya Wilaya ya Tunduru. Hospitali ya Wilaya ya Tunduru ni ya muda mrefu sana ambayo inahudumia karibu Halmashauri mbili zenye zaidi ya Kata karibu 54; na unapoambiwa Kata zaidi ya 54 kwa Wilaya ya Tunduru ni eneo la kilometa za mraba nyingi mno kiasi ambacho kutoka kituo kimoja mpaka kufika Hospitali ya Wilaya ni parefu mno.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe miundombinu ya Hospitali ya Wilaya ya Tunduru iweze kuboreshwa ili wale wote wanaopata huduma katika hospitali ile waweze kupata huduma stahiki. Ingawaje sasa katika hospitali hiyo kumekuwa na mrundikano mkubwa sana wa wagonjwa kiasi ambacho hospitali inazidiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wakati tunaendelea kufanya miundombinu mingine, nadhani tuanze na hii Hospitali ya Wilaya tuiangalie ili tuweze kupata theatre; theatre ipo lakini ipanuliwe zaidi ili kuendelea kuboresha huduma hizi. Pia madawa na vifaa tiba viongezeke mara dufu ya vile vinavyotolewa sasa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii, kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi, aidha nipende kuchangia katika Wizara hii ya Waziri Mkuu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi, ninaipongeza Serikali yangu ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wetu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa mipango mizuri ya kuinua uchumi katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma hotuba ya Waziri Mkuu, kimsingi inaonyesha ukusanyaji wa mapato umepanda toka shilingi bilioni 850 mpaka trilioni 1.2, hii ni hatua nzuri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze udhibiti na usimamizi bora katika haya yafuatayo:-
(i) Matumizi bora ya fedha inayopatikana;
(ii) Kuziba mianya ya rushwa ambayo ilikuwa imekithiri;
(iii) Kukomesha ubadhirifu wa mali ya umma kwa kuchukua hatua stahiki; na
(iv) Wizi wa mali ya umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hiyo imeleta imani kubwa sana kwa Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto kubwa sana katika afya, elimu, miundombinu, kilimo. Katika mkoa wangu wa Ruvuma ambao unajumuisha Wilaya sita zenye jumla ya majimbo tisa ambayo ni kama ifuatavyo; Songea Mjini, Peramiho, Madaba, Namtumbo, Tunduru Kusini, Tunduru Kaskazini, Mbinga, Mjini, Mbinga Vijijini, Nyasa.
(i) Upungufu wa madarasa baada ya sera ya elimu bure kutekelezwa; (ii) Vifaa vya kufundishia;
(iii) Madeni ya walimu; na
(iv) Nyumba za walimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa afya ndipo penye changamoto lukuki, hapa nitaeleza chache na nyingine nitachangia kwenye Wizara ya Afya:-
(i) Kuna kituo cha afya cha Mjimwema katika Manispaa ya Songea kinahudumia wananchi wengi sana lakini mgao wa dawa wanaopata ni mdogo sana, je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza mgao wa dawa ikiwa ni pamoja na kukamilisha vifaa vya chumba cha upasuaji ili
akinamama ambao wanakufa kwa kukosa huduma za upasuaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo hicho cha Mjimwema kipo kwenye mchakato wa kupandishwa hadhi kuwa Hospitali ya Wilaya tangu mwaka jana, ni lini mchakato huo utakamilika?
(ii) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kituo cha afya cha Lusewa (Mji Mdogo) Wilayani Namtumbo ambacho hakina gari la wagonjwa wala vifaa vya upasuaji. Kituo hicho kiko katika jiografia ifuatayo:-
(a) Kutoka Lusewa - Namtumbo - kilometa 80;
(b) Kutoka Lusewa - Songea Mjini - kilometa 150; na
(c) Kutoka Lusewa - Mbesa Wilayani Tunduru - kilometa 150
Mheshimiwa Mwenyekiti, adha wanayoipata wananchi wa Lusewa ni kubwa mno na inatia huruma sana, nimeshuhudia mama anayejifungua akibebwa katika tenga mithiri ya nyanya katika pikipiki akiwa anasafirishwa kilometa 150 toka Lusewa. Pata picha halisi ni maumivu kiasi gani
anayopata mama huyo, hivyo basi akina mama wengi sana wamepoteza maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba yafuatayo kupitia kituo hicho cha afya cha Lusewa; gari ya wagonjwa, vifaa vya upasuaji, dawa na vifaa tiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya miundombinu katika Mkoa wa Ruvuma bado ni tete. Barabara ya kilometa 124 - Lokujufusi - Mkenda bado haijaanza kutengenezwa kwa kiwango cha lami, barabara ya Lumecha - Londo Morogoro bado haijaanza, barabara ya Minga -Nyasa kilometa 66 bado haijaanza, bara bara ya Kitahi - Lituhi bado haijaanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mpainduzi kupitia ATCL imenunua ndege sita, kati ya hizo mbili zimeshawasili na zimeshaanza usafirishaji kwa abiria katika mikoa mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini ndege (usafiri wa anga) utaanza kutoa huduma katika Mkoa wangu wa Ruvuma? Ikumbumbwe kuwa wananchi wa Mkoa wa Ruvuma nao pia ni miongoni mwa Watanzania ambao wanahitaji usafiri wa anga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa usafiri huu wa anga kupitia shirika letu la ndani la ATCL lianze safari Ruvuma kabla hizo ndege hazijachakaa au kabla ya Bunge hili la bajeti kuisha.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa kilimo pia kuna changamoto zituatazo; upungufu wa mbolea ya ruzuku, mbegu zinazoletwa nyingine ni fake, pembejeo za kilimo kutokufika kwa wakati katika vituo vinavyotoa huduma, masoko ya uhakika na upungufu wa mitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikisimama mara kwa mara kuomba Wizara ya Kilimo kuleta huduma ya kibenki kwa maana ya Benki ya Kilimo ili kukuza mitaji ya wakulima wa Ruvuma ili waweze kupata fursa ya kukopa na kukuza mitaji yao na kufanya kilimo chenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaimani unatambua kuwa Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa mikoa yenye mvua ya uhakika hivyo hitaji la benki ni muhimu ili kusaidia wananchi waweze kuzalisha kwa wingi kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania, kwa sababu wakizalisha kwa wingi itakuwa neema kwa Watanzania wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya maji katika Mkoa wa Ruvuma ni kubwa sana, wananchi bado wanakosa maji safi na salama. Kuna miradi ya maji ambayo ilijengwa na World Bank, miradi hii kwa taarifa za maandishi inaonekana imekamilika lakini kiuhalisia maji hayatoki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii ya maji ya World Bank imetumia fedha nyingi sana lakini haijazaa matunda. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha miradi hii inakamilika na inatoa maji? Miradi hii ipo katika Wilaya ya Namtumbo, Mbinga Vijijini na Tunduru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishauri Serikali yangu iendelee kuangalia vipaumbele kwa wananchi ikiwemo maji na kwenye maeneo ya vijijini vichimbwe visima virefu wakati mchakato wa maji ya mtiririko unaendelea basi wananchi waanze kutumia maji ya visima virefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishauri Serikali yangu haya yafuatavyo; zahanati na vituo vya afya vikamilishwe, vifaa tiba na dawa katika vituo vya afya vizingatiwe, pembejeo za kilimo zifike kwa wakati katika vituo vya kusambazia pembejeo, utafiti wa mbegu bora uzingatiwe ili kuleta tija kwa wakulima, ujenzi wa barabara zote nilizoainisha kwa kiwango cha lami, mawasiliano ya simu katika tarafa ya Wino kupitia Halotel ufanyiwe kazi haraka, vita dhidi ya dawa za kulevya uendelee, kulipa stahiki za walimu na madeni ya ndani yalipwe kwa watoa
huduma za ndani (wazabuni).
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha na ninaomba pia mchango wangu huu wote uingie kwenye Hansard.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema na mwingi wa utukufu, kwa kunijalia uzima siku hii ya leo na hatimaye kuweza kusimama hapa ili nami niweze kuchangia Bajeti ya Ofisi ya Rais TAMISEMI na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma vizuri Bajeti ya TAMISEMI, ni nzuri sana. Ukiisoma inaleta raha, ambayo kimsingi Wizara hii inahitaji pesa takribani shilingi trilioni 6.8.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mwaka huu wa fedha tunaokwenda 2017/2018 baada ya kuwa Bajeti ya msimu uliopita imetekelezwa kwa asilimia 75.
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kabisa changamoto kwa msimu uliopita zilikuwa nyingi, basi Wizara hii ijipange vizuri kuhakikisha kwamba bajeti hii inayokuja sasa iweze kutekelezeka kwa asilimia 100.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye asilimia 10 za vijana na wanawake ambazo zinatolewa kutokana na mapato ya ndani ya Halimashauri zetu kwenye maeneo mbalimbali hasa kwa Mkoa wetu wa Ruvuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC, ambaye nimekuwa nikiona kwa macho yangu mwenyewe namna gani jambo hili linatekelezwa kwenye Halmashauri mbalimbali. Jambo hili limechukuliwa tu kama ni jambo ambalo siyo muhimu sana kwa sababu bado
halijatungiwa sheria; likitungiwa sheria mahususi itasaidia hawa Wakurugenzi kuona kwamba ni muhimu na watalitekeleza kwa asilimia 100.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo naipongeza sana Kamati ya LAAC lakini pia na CAG ambaye anatusaidia kukagua hayo mahesabu na kuona hali halisi.
Kamati hii imesimamia vizuri na sasa hivi Halmashauri zote zimeanza kupeleka pesa asilimia tano kwa vijana na asilimia tano kwa wanawake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Wakurugenzi wote ambao wameanza kutekeleza jambo hili na ninaomba waendelee kufanya hivyo na wale wote wanaopewa fedha hizo wasidhani kama ni zawadi, basi hii ni kama Revolving Fund, inatakiwa ipelekwe kwa wengine na wengine waweze kufaidi baada ya wengine kurejesha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye posho za Madiwani. Waheshimiwa Wabunge wenzangu pia wamesema kwamba Madiwani ndio wale ambao wanafanya kazi hasa moja kwa moja kwa wananchi na sisi tukiwa wakati mwingine tunatekeleza majukumu yetu katika
vikao mbalimbali vya Bunge, nao siku zote wamekuwa na wananchi; wakiamka asubuhi wapo na wananchi majumbani kwao. Sisi wakati mwingine tunaweza tukasema, nimesafiri nimeenda huku, lakini wao wanafanya kazi moja kwa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilidhani Serikali yetu ione uhumimu wa kuwaongezea posho Waheshimiwa Madiwani. Wizara hii ya TAMISEMI, tafadhali sana, naomba hata kama kuna sheria au kanuni basi ziletwe hapa Bungeni tuzirekebishe ili nao waweze kufanya kazi wakiwa wakiwa na mori mzuri ambapo kimsingi watakuwa wamewezeshwa vizuri lakini pia waweze kupatiwa vitendea kazi kwa maana ya usafiri.
(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yao ya utawala wakati mwingine unakuta Madiwani wengine wapo vijijini, anatembelea vijiji karibu vinne au vitano; ataenda kwa baiskeli au kwa mguu. Basi Serikali ione umuhimu wa kuwatafutia hata magari ili waweze kufanya kazi zao vizuri.
(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika TAMISEMI pia kwa masikitiko makubwa sana, bado Wizara hii ya TAMISEMI na Utawala Bora pia niseme hamjaona umuhimu wa Mbunge Viti Maalum. Mbunge wa Viti Maalum anafanya kazi kubwa sana. Eneo lake la utawala ni la Mkoa mzima, lakini bado kwa mujibu wa kanuni, Mbunge wa Viti Maalum yeye ni Diwani wa Halmashauri anayotoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza, Mbunge huyu hawezi kuingia kwenye Kamati ya Fedha na kuweza kuona changamoto zinazowakabili wanawake, wanatengewa fedha kiasi gani ili ziweze kuwafikia. Nani anawasemea huko ilihali sisi Wabunge wa Viti Maalum ndio
tupo kwa mujibu ili kuwasemea wanawake wenzetu, lakini kwenye Kamati za Fedha hatuingii? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ya Utawala Bora, muone umuhimu wa kufanya hili na TAMISEMI pia tunataka Wabunge wanawake waingie humo na wanawake Madiwani wa Viti Maalum waingie humo ili waweze kuwasemea wanawake wenzao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa walimu. Katika Mkoa wangu wa Ruvuma, walimu wanapata shida sana, wanafanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha mtoto ambaye hajui ‘a’ wala ‘be’ anafikia mahali ambapo anaweza kusoma na kuandika. Hii kazi ni kubwa sana.
Hata wewe Mheshimiwa Waziri ulioko hapa, nawe ulianzia a, be, che. Kwa hiyo, kumbuka, kama mwalimu yule asingeweza kukufundisha akawa na mazingira mazuri, ni wazi kwamba wewe usingefikia hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara ione umuhimu wa walimu kuwezeshwa wakawa na mazingira mazuri ya kufanyia kazi. Pia walimu wangu wa Mkoa wa Ruvuma wote katika Wilaya zote, nikianza na Nyasa, Mbinga, Tunduru, Namtumbo, Songea Vijijini na
Songea Mjini hawa wote wana madeni. Madeni yao yanafikia takribani shilingi bilioni tatu. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind-up aniambie hawa walimu wanalipwaje hizo pesa zao? Mimi na wewe tutakuwa sambamba, vinginevyo Mheshimiwa Waziri nitakama shilingi
ya mshahara wako. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa kwenye shule za sekondari. Kuna shule za sekondari zinazoanza katika Wilaya ya Namtumbo, ndiyo zinaanza kidato cha tano. Shule hizi zimetelekezwa, hazipelekewi fedha kwa ajili ya mahitaji mbalimbali katika shule hizo ni Nanungu sekondari iliyoko katika Wilaya ya Namtumbo pamoja na shule ambayo inayoitwa Pamoja sekondari, shule ya Namabengo na shule ya Nasuri. Shule hizi zimetelekezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri wa TAMISEMI, tena bahati nzuri Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI tulienda wote katika shule ya Nasuri katika Kata ya Namtumbo, ulishuhudia pale, lakini wale watoto uliwaona wameng’aa kwa uso, lakini ndani yake hawana huduma za
mzingi. Naomba tafadhali utakapokuja, uniambie hawa watoto wanapataje huduma?
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la utawala bora. Nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wangu wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania; na hili nitalisema wazi wazi na nitatembea kifua mbele nikilisema. Mimi kama Mbunge wa Chama cha
Mapinduzi, nataka niwaambie kwamba Mheshimiwa Rais wangu anafanya anafanya kazi nzuri. Ninacho cha kusemea ninaposimama hapa, kwamba ameweza kudhibiti mianya ya rushwa; lakini pia ameweza kupambana na madawa ya kulevya; amerudisha nidhamu kwa watumishi wa umma; bado ameweza kusimamia na kudhibiri matumizi ya fedha katika nchi yetu. (Makofi)
Ndugu zangu, kwa wale wote wanaoitakia mema nchi hii ni lazima watasema kwenye jambo hili. Tunaweza tukasema wakati wowote ule kwa sababu tunajua kwamba Rais wetu anatekeleza na anasimamia vizuri ilani, licha ya shughuli nyingi anazokuwa anazifanya ikiwepo pamoja na
ndege ambazo zimekuja. Nchi hii ilikuwa haina ndege, ni nchi iliyokuwa inatia aibu, lakini kwa kipindi kifupi cha mwaka mmoja na nusu, tayari tumeona ndege, usafiri wa anga unakwenda barabara. Maeneo mbalimbali viwanja vinaendelea kurekebishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili mimi nitalisema tena kwa kifua mbele. Wale wanaochukia na wajinyonge tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba, Mheshimiwa Rais wangu wa Jamhuri ya Muungano, kwa haya aliyoyafanya ya kuweza kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya na mengine, ni lazima…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema na mwingi wa Utukufu aliyenijalia kusimama hapa siku hii ya leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii nami kuchangia Wizara ya Miundombinu. Nianze na usafiri wa anga. Nachukua nafasi hii kumpongeza sana Rais wangu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri ya kusimamia kikamilifu utekelezaji wa ilani, lakini pia kuwezesha ndege hizi sasa kuweza kufanya usafiri ndani ya nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa leo nikiwa nina furaha sana na niwashirikishe Wabunge wenzangu kwamba keshokutwa tarehe 30 ni siku maalum kabisa ambapo ndege aina ya bombardier itaanza safari zake kutoka Dar es Salaam kuelekea Songea. Naishukuru sana Serikali yangu, kitu kama hiki kilikuwa ni ndoto, lakini kwa kudra za Mwenyezi Mungu na kwa jitihada za Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli imewezekana kwa kipindi kifupi cha mwaka mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye barabara. Kuna barabara ambayo ina changamoto kubwa sana. Barabara hii ni barabara yenye urefu wa kilometa 66 inayotoka Mbinga kwenda Mbamba Bay. Naomba barabara hii sasa ianze kutengenezwa kwa sababu ina muda mrefu, imekuwa katika mpango lakini pia tayari upembuzi yakinifu umeshafanyika, ianze kutengenezwa sasa kwa kipindi hiki cha mwaka 2017/2018 ili kuweza kuunganisha mkoa mzima na hata kufikia kule katika Ziwa letu la Nyasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapo sasa tutakuwa tumeshawezesha ile Mtwara Corridor kuwa tayari imeungwa kutoka Mtwara mpaka kufika Mbamba Bay ambapo sasa tunaweza tukasafirisha bidhaa mbalimbali kwa kutumia usafiri wa maji kutoka Mtwara na hata kupeleka mpaka Malawi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niende kwenye barabara ya Likuyufusi. Barabara ya Likuyufusi – Mkenda ni barabara yenye urefu wa kilometa 24 na ni barabara ambayo inaunganisha Mkoa wa Ruvuma na nchi yetu ya Msumbiji; kwa maana ya nchi ya Msumbiji na nchi yetu ya Tanzania. Ni barabara ambayo ikishajengwa kwa kiwango cha lami, itainua uchumi wetu wa Tanzania kwa kuunganisha mipaka hii miwili na kufanya biashara kama nchi marafiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende pia kwenye barabara ya Kitahi – Lituhi – Mbamba Bay. Hii barabara imekuwa ikipigiwa kelele sana, lakini kwa masikitiko makubwa, sijaona ikitengewa pesa kwa kipindi cha mwaka huu 2017/2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii inasikitisha sana na hii ni barabara muhimu ambayo kimsingi kama mnasikia makaa ya mawe yanayochimbwa katika Mkoa wa Ruvuma, basi barabara hii ni ile inayotoka Kitahi kwenda mpaka kwenye yale machimbo na kufikia Lituhi na hatimaye kwenda kuunganisha mpaka Mbamba Bay; inapita kwenye uwanda pembezoni mwa Ziwa Nyasa mpaka kufika Mbamba Bay. Mbamba Bay ni mahali ambapo tayari sasa hivi kumeshakuwa na uwekezaji mkubwa wa mambo ya utalii, lakini nashangaa hii barabara haiunganishwi hata kuweza kuwezesha watalii kuweza kufika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ina umuhimu mkubwa na ukizingatia kwamba magari makubwa yanayokwenda kuchukua makaa ya mawe kule katika eneo lile linalochimbwa makaa ya mawe; ni magari ambayo yanatimua vumbi kiasi ambacho wananchi wanaoishi pembezoni mwa zile barabara tayari asilimia kubwa wanaathirika kutokana na zile vumbi, wanapata maradhi ya aina mbalimbali, lakini pia inachelewesha hata namna ya kutoa makaa ya mawe na kupeleka labda Mtwara kule ambako huyu mwekezaji ambaye anazalisha cement kwa wingi anachukua makaa ya mawe kule. Siyo huko tu, viwanda vyetu vingi sasa hivi vinatumia makaa ya mawe. Kwa hiyo, barabara ile ni muhimu ili kuweza kurahisisha uchumi wetu tunaoutarajia; uchumi wa kati kufikia mwaka 2025. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara nyingine ya Lumecha – Londo. Barabara hii inaunganisha Mkoa wa Ruvuma na Morogoro. Barabara hii toka tumeanza kuiimba, ni muda mrefu na sijaona kama imetengewa pesa. Namwomba Mheshimiwa Waziri, tafadhali sana naomba atenge pesa kwa ajili ya kuunganisha hii barabara inayotoka Lumecha hatimaye kwenda Londo, Mkoa wa Morogoro. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ambayo inatoka Mtwara Pachani kuelekea Narasi. Barabara hii kwa kweli wanasema hivi, mtu naweza akasahau kwake, akapata sungura wa kugawa, akagawia maeneo mengine akasahau kwake. Namwona kabisa kaka yangu Mheshimiwa Ngonyani Naibu Waziri wa Miundombinu amesahau; na leo nimeona nisimame hapa niisemee. Barabara hii iko katika Jimbo lake lakini naona kama ameisahau. Naomba Mheshimiwa Waziri tafadhali juu ya tafadhali, naomba utusaidie hii barabara ili iweze kutengenezwa kwa kiwango cha lami iweze kusaidia wananchi wa Namtumbo lakini pia na wananchi wa Tunduru. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii imeweka changamoto nyingi sana kiasi ambacho akinamama wengi wanaopata shida za namna ya kujifungua kwa kweli siku ya uwasilishi hapa wa Wizara ya Afya, jamani nitawaletea na picha ili mwone wanawake wa Namtumbo wanavyopata shida hasa maeneo ya kule pembezoni kuelekea Namtumbo na kuunganisha na Tunduru. Wanapata shida kubwa sana kiasi ambacho wanabebwa mpaka kwenye matenga, barabara ni shida, magari hayawezi kwenda huko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri barabara hii. Naomba sana Mheshimiwa Waziri amsaidie ndugu yake huyo Naibu Waziri aliyeko hapo ili aweze kupata hii barabara. Barabara hii ina changamoto kubwa sana; akina mama wanapoteza maisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hebu siku moja hawa wanaume na wenyewe wangeonjeshwa wakaona uchungu wa kuzaa, ndiyo pale wangeweza kujali na kuthamini hata wakaona umuhimu kwa barabara ambazo tunaziomba kwa machungu waweze kutuunganishia. Akinamama wanapoteza maisha! Nasikia uchungu sana, natamani kulia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ambayo inatoka Lingusenguse kuelekea Tunduru, nayo ni ya Mheshimiwa Naibu Waziri katika Jimbo lake. Anashindwa kusema, mimi naona nimsemee hapa kwa sababu yeye yuko hapo. Naomba umsaidie hii barabara pia ina changamoto kubwa. Tafadhali juu ya tafadhali, tusaidieni, wanawake wa Namtumbo wanapoteza maisha, wanawake wa Tunduru wanapoteza maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niende kwenye barabara ya Nangombo – Chiwindi yenye urefu wa kilometa
19. Barabara hii ni barabara ambayo iko kwa dada yangu Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya, anafuatilia pole pole, lakini mimi leo nimesimama hapa kindakindaki nimsaidie kumsemea mwanamke mwenzangu. Barabara hii nayo ina changamoto kubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba barabara hizi nilizozitaja hapa zilizopo ndani ya Mkoa wa Ruvuma, endapo zitatengewa fedha, katu hutaniona nikisimama hapa nikiongelea barabara tena katika Mkoa wa Ruvuma. Kwa maana moja ama nyingine, tutakuwa tumemaliza matatizo ya barabara katika Mkoa wa Ruvuma. Naomba tafadhali sana mwaka huu wa fedha muweze kutenga fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia barabara hii niliyosema ya Kitahi – Lituhi, Mheshimiwa Waziri kama hataitengea fedha atakapokuja ku-wind up hapa, haki ya Mungu nitashika shilingi. Nimhakikishie kabisa nitashika shilingi kwa sababu ni barabara ambayo ni muhimu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kwamba nakushukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini pia kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii. Nikupongeze sana kwa namna unavyofanya kazi ya kuliongoza Bunge hili, kwa umahiri mkubwa ikiwa ni pamoja na timu yako. Hongereni sana, chombo kinakwenda barabara, tumeridhika na utendaji wako wa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuchangia hotuba ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na nitakwenda moja kwa moja kwenye haki za wasanii. Naomba niongelee tu kwenye eneo hili la wasanii. Wasanii wetu wa Tanzania wanafanya kazi nzuri. Moja kati ya kazi kubwa ambayo wanaifanya ni pamoja na kuitangaza nchi yetu. Wako wasanii wazuri ambao wanafanya vizuri kwenye michezo kwa maana ya mpira wa miguu lakini pia kwenye kuimba na mambo kadha wa kadha.

Mheshimiwa Spika, napenda niwatambue baadhi ya wasanii hapa ambao wanafanya vizuri kwa mfano, Mzee Jongo, Ray, Diamond, Khadija Kopa, Ali Kiba, Profesa Jay na kijana mmoja machachari sana ambaye anawakilisha Mkoa wa Ruvuma yuko katika Bendi ya TOT anaitwa Neka, kijana huyo anatoka katika Wilaya ya Namtumbo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawa wasanii wetu ni vizuri kabisa tukahakikisha kwamba wanapata haki zao za msingi ili kuweza kufanya usanii wenye tija. Inaonesha kwamba hawa wasanii kumekuwa na sheria ambayo inawabana. Wakati mwingine wanapenda kurekodi video zao ili watengeneze kanda lakini wanakuwa wanabanwabanwa, kwa mfano, labda anahitaji kwenda kurekodi kwenye eneo la daraja lile la Kigamboni, visheria vinawabanabana wanashindwa kufanya hivyo. Wakati mwingine wanatamani hata watumie labda gari la polisi kwa ajili ya kurekodi lakini wanashindwa kufanya hivyo, lakini wakitoka hapa wakaenda nchi za wenzetu wanapewa ushirikiano wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, naomba kama kuna sheria inawabana kutumia vitu hivyo basi tuweze kuileta hapa tuirekebishe ili wapate haki za msingi za kuweza kufanya recording ambayo itawasaidia na watakuwa wanafanya uwekezaji wenye tija kwenye usanii huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende pia kwenye suala la usikivu wa TBC. Kule kwetu Nyasa bado TBC haisikiki vizuri. Namwomba Mheshimiwa Waziri afanye kazi ya ziada, kwa sababu mpaka sasa hivi tunasikiliza habari za Malawi. Kuna ka-station fulani ya ka-Malawi kanachezacheza pale, sisi hatutaki, sisi sio wa Malawi, sisi ni Watanzania, weka TBC, acha maneno, weka muziki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi alisimama Mbunge mmoja hapa, nadhani matatizo ya kwenye jimbo lake yamekwisha kabisa hata wananchi wake wamekuwa wana hali nzuri kiasi ambacho hawana changamoto yoyote amejikuta anaacha kushughulikia mambo ya jimbo lake anaenda kushughulikia mambo kama ya shilawadu. Amesimama hapa akiongelea suala la Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi kufichwa, mimi nashangaa sana Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi amefichwa wapi au kutekwa kwa namna moja au nyingine wakati huyu Katibu Mkuu yuko Arusha. Naomba niseme haya hayamhusu, ashughulike na ya kwake yanayomhusu. Pia huyu Kinana ni Katibu sio wa lelemama huwezi kumlinganisha Katibu huyu wa Chama kikubwa Chama cha Mapinduzi ukamlinganisha na Makatibu wa vyama ambavyo vinafanana na SACCOS fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kanali Mstaafu Kinana ni kiongozi mzuri, ni mwamba wa vita, ni mpiganaji hasa hasa kwenye Chama chetu cha Mapinduzi. Pia ni mkweli, ni mchapakazi na hana uwoga kwenye kusemea Chama chake cha Mapinduzi. Sasa nashangaa ukamchukua Kinana unamlinganisha na chama chake na wala nisimfiche ni Mheshimiwa Lema, anamlinganisha Kinana gwiji la siasa, mwanaume kabambe ambaye anaweza kusimamia Chama cha Mapinduzi ipasavyo na Katibu wake ambaye haeleweki kama yuko duniani au yuko akhera mpaka sasa hivi, hii inasikitisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshauri tu kaka yangu Lema na mimi niseme toka nimefika hapa nimeanza Bunge hili la Kumi na Moja sijawahi hata siku moja kusikia akiongelea masuala yanayohusu jimbo lake amejikita kwenye mambo ya diplomasia ya kitaifa na kama nasema uongo rejeeni Hansard zake zote mtaona. Niseme hivi kwamba kama anahitaji aje tu CCM wala hatuna hiyana tutampokea lakini hii kutafuta chokochoko sio njema.

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Jimbo hilo la Arusha, naomba nimshauri kaka yangu Lema ajikite huko, watu wa Arusha bado wana changamoto kubwa sana wanahitaji wasemewe na Mbunge wao, badala yake yeye amejikita kwenye mambo ya ushilawadu na kwenye mambo ya unabii…

Mimi niseme kazi ya unabii siyo yake kwa sababu ni nabii wa uongo.

Mheshimiwa Spika, alitabiri hapa Dkt. John Pombe Magufuli atakufa na hajafa, ndio kwanza anaendelea kutekeleza majukumu yake, kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ipasavyo na maendeleo yanaonekana. Kazi anazozifanya Dkt. John Pombe Magufuli…

Ni kazi nzuri na wanachi wote wanazikubali.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, unabii wake ni wa uwongo na mimi leo nataka nimbatize jinaJina ninalombatiza leo hii ni nabii Israel mtoa roho za watu.
TAARIFA...

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na ndiyo maana nimesema uko vizuri na unachapa kazi ipasavyo na tunakubaliana na utendaji wako wa kazi. Kwa sababu wako watu sasa wanashindwa kujitambua nini aseme hata ulivyokuwa unajaribu
kumfundisha, tunakushukuru umekuwa mwalimu kwetu, umemfundisha hapa msemaji mmoja alikuwa anaongelea vyeti, mara ooh siyo lazima uwe na vyeti, mara nini, haeleweki, Mbunge wa Ubungo umemfundisha hapa vizuri lakini unaendelea kutoa hiyo elimu hata Mwalimu na yeye umemfundisha vizuri. Tunakushukuru sana na tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu endelea kuchapa kazi tuko nyuma yako tunakuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiyo taarifa siipokei kimsingi amenipotezea muda na naomba unilindie dakika zangu, nina mambo ya msingi sana ya kuchangia hapa. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kwa utulivu sana kumpongeza sana Waziri mwenye dhamana ya habari. Sina mashaka na utendaji wake wa habari, sina mashaka na utendaji wake wa kazi, ni Waziri mahiri, ni Waziri ambaye ameshafanya kazi Wizara mbalimbali na kila eneo alilopewa kufanya kazi amefanya vizuri. Kwa hiyo, ni matumaini yangu atawatendea haki wasanii wa nchi hii na ataitendea haki Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba niwatie moyo Mheshimiwa Waziri, Naibu pamoja na timu yako yote fanyeni kazi. Hizi kelele za chura hazimzuii mwenye nyumba kulala, wala kelele za chura hazimzuii chura kunywa maji, kwa hiyo endeleeni kuchapa kazi, tuko nyuma yenu tunawaunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno haya, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, mwingi wa Utukufu ambaye ameniwezesha kusimama hapa siku hii ya leo nikiwa na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nianze na barabara ya kilometa 130 ambayo inatoka Kitai kwenda Mbambabay. Barabara hii ni ndefu, lakini kulingana na changamoto ambayo iko katika barabara hiyo ya kipande cha kilometa 40 inayotaka Kitai kwenda mpaka pale Rwanda kwenye uchimbaji wa makaa ya mawe, mimi naomba Serikali ichukue kipande hiki cha kilometa 40 kwa maana ya changamoto yake, ili iweze kurahisisha uchimbaji wa makaa ya mawe na usafirishaji wake. Kilometa 40 hizi zitasaidia sana kurahisisha utekelezaji huu wa uchimbaji wa makaa ya mawe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niende kwenye suala la maji, wanawake wenzangu wa Mkoa wa Ruvuma wanapata shida sana kwenye eneo hili la maji. Maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Ruvuma bado yana shida kubwa ya maji. Inawezekana kabisa asilimia chache sana za upatikanaji wa maji, naomba suala hili Serikali ilichukue na kuhakikisha kwamba maeneo yote ya Mkoa wa Ruvuma wanawake wenzangu wanapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika niseme kuna Benki ya Kilimo. Benki ya Kilimo hata mwaka jana nilisimama hapa. Benki ya Kilimo imekwenda kuwekwa kwenye maeneo ambayo mengine hayana walengwa sahihi wa masuala ya kilimo.

Ninaomba benki hii ya kilimo, nilisimama mwaka jana Mheshimiwa Mpango, nikakamata na shilingi yako ukaniahidi kwamba mimi hii ni bajeti yangu ya kwanza, naomba uniachie ili mimi nitahakikisha kwamba mwaka huu wa fedha Benki ya Kilimo inakwenda Ruvuma. Mpaka leo ng’oo hakuna Benki ya Kilimo, sasa sijui nikueleweje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba utakapokuwa unakuja ku wind up hapa unieleze benki hii inaanza lini? Kama shida ni majengo basi mimi nitawapa jengo langu ili wakae pale wafanye kazi hiyo. Tafadhali naomba ili wanawake waweze kukopa mikopo na wananchi wengine wote waweze kukopa mikopo waweze kufanya kilimo chenye tija ambacho kitawasababisha wapate mitaji mizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye kodi ya nyumba. Kodi ya nyumba ni nzuri, hata mimi mwaka jana nilisimama hapa nikapongeza Serikali kuchukua uamuzi wa kuipa TRA iweze kukusanya pesa hiyo kwa maana ya kodi ya majengo. Lakini sasa naona kwamba yaani napata picha namna gani ambavyo utakwenda kwa mwananchi ukasimama pale akamwambia akupe shilingi 10,000 ya pamoja ni maumivu, na inawezekana kabisa utekelezaji wake utakuwka na rabsha mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mawazo yangu ni kwamba, kwenye ile tozo ya shilingi 40 tuliyoiweka tungeongeza tozo ya shilingi 50 ili iingie huko na watu waweze kulipa kodi hii bila maumivu ya moja kwa moja wanayoyaona. Na ninaamini kabisa hili litatekelezeka bila kelele zozote. Lakini pia tutenganishe nyumba, nyumba ziko za biashara na nyumba za makazi. Kwa hiyo, wale wa biashara basi wachukuliwe kibishara na hizi za makazi iongezeke tozo ya shilingi 50 ili waweze kulipa kwa mtindo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naenda kwenye afya. Niombe sana, kuna maeneo ambayo wakati wa Wizara ya TAMISEMI nilichangia hapa. Nikaainisha maeneo ya Namtumbo kule, kwenye Kituo cha Afya cha Rusewa, tunahitaji gari la afya, ambulance kwa ajili ya kurahisiha wanawake ambao wanakwenda kujifungua kutoka pale Rusewa kwenda kule katika Wilaya ya Tunduru. Kuna eneo ambalo lazima watembee kwa kilometa 150 ambalo wanakwenda kubebwa kwenye matenga. (Makofi)

Mheshimiwa Rais uliko huko naomba unisikie na mimi naomba ambulance moja ili iende kule Namtumbo ikasaidie wanawake wa Namtumbo katika Mkoa wa Ruvuma. Nakuomba sana baba yangu, pamoja na jitihada zote na kazi zote unazoendelea kuzifanya basi na hilo naomba wanawake wa Ruvuma kule, walikutwangia kura nyingi sana za kishindo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nizungumzie wazabuni wa ndani. Wazabuni wa ndani kama wa mawakala wa pembejeo wamekuwa wakinyanyasika mpaka sasa hivi hawajalipwa pesa zao, naomba Serikali ione umuhimu. Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli wewe ni Rais wa wanyonge, unagusa kabisa matatizo ya wanyonge. Waone hawa wazabuni ambao wamekuwa wakihangaika mpaka sasa hivi hawajui hatma yao, wasaidie ili waweze kupata haki yao. Wale ambao hawajafanya vizuri wawekwe pembeni, waliofanya vizuri kwa uaminifu walipwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika wazabuni wa ndani, kwa mfano wako waliohudumia mashule, vyuo, lakini pia wapo waliohudumia kwenye vikosi vya jeshi, nao pia waweze kulipwa hizo pesa ili waweze kuendeleza mitaji yao. Tunahitaji uchumi wa viwanda wakati watu wetu wa ndani tunawaumiza na kuwaangamiza na kuua mitaji yao, tuwalipe waendeleze shughuli zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo anatekeleza majukumu yake na kubainisha matatizo moja baada ya lingine na kuyaondoa kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumza hapa masuala ya makinikia. Makinikia yamezungumzwa na Wabunge wengi, lakini juzi mmemsikia Mbunge alizungumza hapa, Mbunge huyu anaitwa Mheshimiwa Heche, alizungumza akawa anahamasisha wananchi wake waende kuvamia migodi, kwa hiyo kazi aliyoifanya na leo anajikosha kwa kuomba mwongozo hapa. Mimi niseme tu hicho ndicho alichokitaka na amesha-organize wameenda kuvamia migodi, Rais hajasema kwamba watu wakavamie migodi, kwa hiyo, huo ni uvunjaji wa sheria, hao watu washughulikiwe kama wahalifu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo mwongozo wako umeelekeza kwamba aende kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, mimi naomba aunganishwe na yeye kama mhalifu namba moja, kwa sababu yeye ndio aliyekuwa anahamasisha hapa ndani tumemsikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie pia suala la Mheshimiwa Tundu Lissu, Mheshimiwa Tundu Lissu anapinga ripoti hii iliyotolewa ya vyombo vya utafiti uliofanyika. Mimi nataka niseme hivi, hawa wajumbe walioingizwa kwenye ile Kamati sio kwamba wanajipangia wao wenyewe, vipo vyombo mahsusi vinavyochuja na kubainisha sifa za watu ili waweze kuingizwa kwenye vyombo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchunguzi uliofanyika ni sahihi na ripoti ambayo imeletwa kwa Mheshimiwa Rais ni sahihi na ninaomba ikumbukwe kwamba uchunguzi unapofanyika na ripoti inapopelekwa maana yake mwenye haki wa hiyo ripoti ni yule ambaye aliagiza ripoti ifanyike ambaye ni Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme, kifo cha nyani kila mti huwa unateleza, imefika mahali hawa wenzetu sasa hata wanayoyasema kwamba Rais anatekeleza waliyoyasema wao, leo hii wanayakataa tuwaeleweje? Lakini pia amesimama Mbunge hapa, ametumia dakika 10 Mbunge wa Arumemeru Magharibi ametumia dakika 10 kulalamikia shamba la maua la Mheshimiwa Mbowe, hivi ni akili ni matope. Wananchi wake hawana shughuli zingine, hawana changamoto ni mambo ya aibu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia alisimama Mbunge hapa akasema sisi Wapinzani ni kioo cha Chama cha Mapinduzi, mimi sikatai, inawezekana kuwa ni kioo, lakini kioo cha sasa hivi cha huo upinzani tayari kina crack hivi mtu utajionaje? Kioo kina ukungu utajionaje, ninyi wenyewe mnaenda mbele, mnarudi nyuma hamjitambui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba lakini pia niseme, kwa maana hiyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vya afya vingi vilivyojengwa kwa nguvu za wananchi Mkoani Ruvuma vingi vimefikia renta, havijaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali itenge fedha kwa ajili ya kumalizia hivyo vituo vya afya ili kuokoa nguvu za wananchi zilizotumika, lakini pia kuboresha huduma ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na Sera ya Taifa ya Elimu Bure kumekuwa na changamoto ya upungufu wa madarasa. Ninashauri Serikali yangu kuweka mkakati madhubuti ambao utalenga kuongeza madarasa katika shule zote zenye upungufu wa madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa walimu mashuleni umekuwa ni kero kubwa sana. Shule nyingi hazina walimu wa kutosha. Kutokuwa na walimu wa kutosha ni sawa na kuandaa chakula kizuri ambacho hakina chumvi. Athari ambayo itajitokeza katika Taifa hili baada ya miaka mitano ni kuwa na kizazi ambacho hakitakuwa na elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu afya, hospitali ya Wilaya ya Mbinga ina upungufu mkubwa wa wodi kwa ajili ya akina mama wanaosubiri kujifungua na wale ambao wameshajifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi, naomba Waziri wa Afya aje katika Hospitali ya Mbinga, Mkoani Ruvuma ajionee mwenyewe adha ambayo wanaipata wanawake hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuongeza bajeti katika sekta ya afya hususani madawa na vifaa tiba, lakini bado madawa hayatoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sanaa, nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupiga marufuku kwa wasanii wanawake kuvaa nguo ambazo ni kinyume na maadili yetu sisi Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba hoja na maoni yangu mbalimbali yaingie kwenye Hansard.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mungu kwa kunipa uzima siku ya leo ili niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na changamoto; kumekuwa na changamoto kubwa sana katika sekta ya afya katika Mkoa wangu wa Ruvuma. Elimu ya uzazi wa mpango bado inahitaji kufikishwa vijijini, vituo vya afya vingi havina maji, vituo vya afya havina magari ya wagonjwa jambo ambalo limekuwa likisababisha vifo vingi vya akina mama na watoto. Wahudumu katika vituo vya afya, manesi na madaktari ni tatizo kubwa.

Kumekuwa na tabia ya baadhi ya wazazi kushirikiana na watu ambao wanawapa mimba wanafunzi kuwaficha wahalifu ambao wamewapa mimba watoto ambao ni wanafunzi. Je, Serikali imeshachukua hatua gani kwa wazazi ambao wanajihusisha na tabia hiyo ya kumdidimiza ntoto wa kike? Je, ni madume wangapi ambao wamefungwa kwa kosa la kumpa mimba mwanafunzi?

Mheshimiwa Naibu Spika, taa za kufanyia operation nazo ni shida, mashine za oxygen hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbinga Mji kuna changamoto ya upungufu wa wodi za wagonjwa hususani wodi za akina mama (wodi ya wazazi),tunaomba Wizara itusaidie kuongeza wodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ni kuhusu mikopo ya akina mama. Wanawake wamekuwa na hitaji kubwa la mikopo lakini hawapati ipasavyo, ipo mikopo inayotolewa na Halmashauri mbalimbali, lakini bado haitoshi. Je, Wizara ina mpango gani wa kuwawezesha wanawake?

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na vitendo vya kikatili ambavyo wamefanyiwa wanawake na watoto, hivi karibuni kuna mtoto ambaye anatembezwa kwenye mtandao ambaye ameshuhudia baba yake akiwachinja wadogo zake mapacha wawili. Napenda kujua kama Wizara inajua jambo hili na kama inajua imechukua hatua gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Wilaya ya Tunduru ina tatizo la kitanda cha upasuaji. Tunaomba Wizara ichukue hatua za haraka ili kuokoa maisha ya wananchi wa Wilaya ya Tunduru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Maji. Pia ninaomba mchango wangu huu wote uingie kwenye Hansard.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai, suala la maji ni muhimu sana katika jamii. Miradi ya maji mingi inayotokana na World Bank ni miradi ambayo imetumia pesa nyingi sana na mingi haijakamilika. Ni kwa nini wahusika katika miradi hii ya maji ambayo haijatekelezeka hawachukuliwi hatua? Iko miradi zaidi ya minne ya fedha za World Bank ambayo haipo katika hali nzuri mkoani Ruvuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuainisha miradi ya maji iliyoko katika Mkoa wa Ruvuma ambayo haijakamilika na kimsingi fedha hizo hazijulikani ziliko kwa kuwa inaonesha fedha zimetumika na miradi haijakamilika kama ifuatavyo:-

(1) Mradi wa Maji Mkako katika Wilaya ya Mbinga ambao umetumia fedha zaidi ya shilingi 600,000,000;

(2) Mradi wa Maji wa Litola Wilayani Namtumbo umetumia fedha zaidi ya shilingi million 700,000,000; na

(3) Mradi wa Maji wa Matemanga Wilayani Tunduru (Tunduru Kaskazini) ambao umetumia fedha zaidi ya 500,000,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, ubadhirifu huu unaofanywa katika Wizara hii kwenye miradi hii ya maji hauvumiliki.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu iundwe Tume ya kufuatilia miradi hii ili tupate majibu sahihi juu ya miradi hii na ufisadi mkubwa uliopo kwenye miradi hiyo. Mimi nilikuwa Mjumbe wa Kamati ya LAAC ninajua vizuri juu ya miradi mbalimbali ya maji iliyoko katika nchi yetu katika mikoa ya Tanga, Mbeya, Iringa na maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye amenijaalia kusimama hapa siku hii ya leo ili na mimi niweze kuchangia hotuba ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakwenda moja kwa moja kwenye suala linalohusu usafiri wa anga. Usafiri wa anga kutoka Mkoa wa Ruvuma kwa maana ya Songea, Mtwara kwenda Dar es Salaam. Tulikuwa tuna usafiri wa anga kwa maana ya ATCL lakini kwa masikitiko makubwa, usafiri huu umeondolewa kwa maelekezo ambayo tumepata kutoka kwenye Wizara kwamba uwanja unafanyiwa ukarabati lakini uwanja huo umetengewa karibu miezi 18 kwa ajili ya ukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona hizi ni siku nyingi sana kwa ajili ya ukarabati na isitoshe usafiri huu umekuwa ukichochea uchumi wa Mkoa wa Ruvuma na Mtwara kwa ujumla. Kwa hiyo, niombe huu ukarabati badala ya kufanyika kwa kipindi cha miezi 18 basi ufanyike kwa kipindi cha miezi sita ili uweze kurahisisha shughuli za wafanyabaishara na wananchi wote kwa ujumla kwenda kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii sasa niende kwenye barabara ambazo ziko ndani ya Mkoa wa Ruvuma kwa maana ya wilaya mbalimbali zilizoko katika Mkoa wa Ruvuma. Kuna barabara ya Madaba – Ludewa inayounganisha Madaba na Ludewa ambayo tayari inaonekana imetengewa pesa na mwaka jana ilionekana hivyo hivyo, lakini bado utekelezaji haujaanza. Niiombe Serikali yangu iweze kufanya hima ili huduma hizi ziweze kufanyika kwa wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ambayo iko Wilaya ya Namtumbo, ya Mtwara – Pachani – Lusewa kwenda mpaka Nalasi. Ahadi hii ilikuwa ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne lakini mpaka sasa hivi naona mpango mkakati unaendelea, mchakato unaendelea bado haijaingia kwenye utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa Mheshimiwa Mbarawa akaze misuli ili hii barabara iweze kutengemaa na wananchi waanze kuitumia kwa sababu inaunganisha wilaya mbili; Wilaya ya Namtumbo na Wilaya ya Tunduru ikipitia kule Nalasi, naomba atusaidie sana. Mwaka jana nilisimama hapa nilisema nitatoa shilingi na kweli nilitoa shilingi, sasa mwaka huu nitaondoka nayo kabisa niende nayo Ruvuma kama hatakuja na muafaka juu ya barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya Namabengo - Mbimbi – Nalwehu yenye urefu wa kilometa 11. Naomba nayo pia iweze kuanza kutekelezwa kwa kipindi hiki cha mwaka 2018/2019. Hizi barabara zote zinapatikana katika hotuba ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ukurasa 220. Kuna barabara ya Lumecha – Kitanda – Londo – Kilosa – Kwampepo, hii barabara nimekuwa nikiimba sana, inaunganisa Mkoa wa Ruvuma na Mkoa wa Morogoro. Tunaomba sana barabara hii iunganishwe itakuwa ni shortcut na itarahisisha sana uchumi kati ya mikoa hii miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niende kwenye barabara ambayo iko katika Manispaa ya Songea, hii ni bypass, ina urefu wa kilometa 11 ambayo ilikuwa katika package ya Mtwara Corridor na inatoka katika Kata ya Sidifamu - Msamala – Ruhiko, ni kilometa 11 tu. Namwomba Mheshimiwa Mbarawa, atupie jicho hapo ili tuweze kupata ile bypass.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu kumekuwa na msongamano mkubwa sana katika Halmashauri ile ya Manispaa ya Songea. Malori yanapita hapo hapo, pikipiki na magari madogo, kwa hiyo, imekuwa ni tafrani, hapakaliki, hapaeleweki. Kwa hiyo, tunaomba tupate hiyo bypass ambayo itasaidia kupumua yale magari angalau hata mjini pale pakaweza kutazamika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende Songea Vijijini kwenye barabara yenye urefu wa kilometa 32 ambayo inatoka Mletele - Matimila - Mkongo. Naomba barabara hii iweze kufanyiwa matengenezo ili iweze kurahisisha pia shughuli za wakulima waweze kusafirisha mazao yao vizuri ipasavyo.
(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima na taadhima, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ubadhirifu katika miradi ya maji. Kwenye miradi ya maji kuna ubadhirifu mkubwa sana. Hii inasikitisha sana pale ambapo Serikali inatoa pesa na pesa zile haziendi kufanya kazi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Litola kuna mradi wa maji wa zaidi ya shilingi milioni 200 lakini mradi ule haufanyi kazi una zaidi ya miaka mitatu. Kata ya Mkako kuna mradi wa shilingi milioni 718, mradi huu maji hayatoki lakini pesa asilimia karibu 90 imeshalipwa kwa mkandarasi. Sasa mimi nashindwa kuelewa hili jambo linakuwaje na wakati huo huo, katika utekelezaji huu huwa kunakuwa na Mhandishi Mshauri, Mhandishi Mshauri ambaye anashauri miradi kama hii hapa ambayo mwisho wa siku inagharimu pesa nyingi na haiwezi kutoa maji na kufikia malengo tunayokusudia amechukuliwa hatua gani? Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa aseme katika miradi hii iliyofanyiwa ubadhirifu ni watu gani ambao wamechukuliwa hatua ili tuweze kujua vinginevyo Mheshimiwa Waziri nashindwa kukuelewa pale ambao upo hapo lakini pia hatusikii chochote kinafanyika kuhusiana na hawa watu waliofanya ubadhirifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri Mbarawa kwamba kuna dhambi ambayo hawezi kuikwepa hata ikawaje. Mkoa wa Ruvuma katika Kata nilizozitaja, Kata za Litola, Mkako, Nandembo ndoa za watu zimevunjika kwa sababu ya kukosa maji. Akina mama wanafuata maji umbali mrefu, kwa hiyo, kuna ndoa ambazo zimevunjika, Kata ya Litola ndoa tatu zimevunjika, Mheshimiwa Waziri atajibu. Kata ya Mkako ndoa tisa zimevunjika, wanawake wanafuata maji umbali mrefu. Kata ya Nandembo hali kadhalika ndoa nne zimevunjika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri hawatendei haki Wanawake wa Mkoa wa Ruvuma kwa sababu sasa wanaondoka kwenye hali ya kuwa na ndoa zao wanaanza kuwa ma-bachelor. Niombe sana utakapokuja unijibu. Naomba sana Mheshimiwa Waziri Mbarawa nisaidie katika hili kuhakikisha kwamba miradi hii niliyoitaja iliyogharimu pesa nyingi, nijue ni nini ambacho kimefanywa kwa sababu katika Mradi wa Mkako, shilingi milioni 718 zinaendelea tu mradi haufanyi kazi, umeacha tafrani katika maeneo husika. Naomba tafadhali sana sana sana, wanawake wa Mkoa wa Ruvuma tunakulilia ndoa zetu zinavunjika kwa sababu ya kufuata maji umbali mrefu, waume zetu wanakosa imani, tunashindwa kuwahudumia waume zetu, kwa hiyo, tunakosa sifa ya kuwa wanawake bora wa kuhudumia familia zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naunga mkono hoja, Mheshimiwa Waziri naomba ajibu kwa nini miradi hii…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na utukufu ambaye amenijalia uzima hatimaye niweze kusimama hapa kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Ruvuma ili niweze kuchangia hotuba ya Waziri wa Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wangu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya. Pia nimpongeze Mama Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu pamoja na Waziri wa Wizara ya Kilimo, wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee, nimpongeze sana Waziri Mkuu namna ambavyo amekuwa akifanya kazi nchi nzima. Kimsingi hamna asiyejua namna anavyotimka kufuatilia sekta ya kilimo na kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wanatendewa haki katika sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi kuishukuru sana Serikali ya CCM inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli kwa namna ambavyo wametutengea ujenzi wa ghala kubwa katika Mkoa wa Ruvuma. Pale Songea Mjini kunaenda kujengwa ghala kubwa ambalo lina uwezo wa kuchukua tani 81,000 za mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba suala hili la ujenzi wa ghala kubwa liende sambamba na hoja kubwa ambayo nimekuwa nikiisema mara nyingi hapa inayohusu pembejeo za kilimo. Kwa Serikali yangu kuona umuhimu wa kujenga ghala kubwa katika Mkoa wa Ruvuma ina maana inatambua wazi namna gani Mkoa wa Ruvuma umekuwa ukizalisha mazao ya mahindi kwa wingi. Katika Tanzania hili ni ghala ambalo linaongoza, hakuna ghala lenye kuchukua tani nyingi kiasi hicho. Kwa hiyo, ujenzi huu wa ghala uende sambamba na suala la pembejeo za kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri kwenye suala la pembejeo za kilimo iongezwe ruzuku hapa kwenye mbolea. Nashauri mbolea ya ujazo wa kilo 50 ikiongezewa ruzuku iende ikauzwe Sh.10,000 kwa kila mfuko. Hii itawasaidia sana wakulima lakini pia itaongeza tija ya uzalishaji katika eneo hili kwa sababu kupeleka tu ghala haitoshi, ni lazima kuwe na mkakati mzuri ambao utapelekea uzalishaji wa haya mahindi kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nadhani ni vizuri Wizara ya Kilimo pia ikafanya jitihada za makusudi za kupeleka Benki ya Kilimo katika Mkoa wetu wa Ruvuma ili wananchi wale waweze kukopa na kuongeza tija kwenye mazao yao kwa maana ya kuongeza mtaji. Nimekuwa nikiuliza hili swali mara nyingi ni lini Benki ya Kilimo itapelekwa katika Mkoa wa Ruvuma lakini majibu yake hayana afya, najibiwa juu-juu tu, ni majibu ambayo hayakidhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kulikuwa na umuhimu sana wa kupeleka hii Benki ya Kilimo tofauti na sasa hivi Benki ya Kilimo imewekwa pale Dar es Salaam, kuna mashamba gani pale Dar es Salaam? Watu wamekaa kwenye viyoyozi, wapo maofisini wakitoka wanaingia kwenye magari wanaenda nyumbani, kwa hiyo, haileti tija kuweka Benki ya Kilimo katika Mkoa wa Dar es Salaam. Peleka Benki ya Kilimo katika Nyanda za Juu Kusini ili wakulima wale waweze kuzalisha mazao kwa wingi kwa sababu ni wakulima haswa wanaofanya kazi za kilimo zinaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niende kwenye suala la masoko. Nimesoma kitabu hiki cha hotuba ya Waziri wa Kilimo, nimekwenda ukurasa wa 75, nilichokiona wanazungumzia kuzalisha katika kilimo lakini pia amezungumzia suala la uhifadhi sijaona akizungumzia suala la masoko ya mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naona kama Nyanda za Juu Kusini tumetengwa kwa maana ya kwamba suala la mahindi halijawekewa mkakati madhubuti ambao utamnyanyua mkulima wa Tanzania ambaye kimsingi amekuwa akizalisha kwa kutumia nguvu nyingi lakini uzalishaji wake hauna tija. Hivi sasa ni mpaka mtu auze madebe matatu ya mahindi ndiyo apate kilo moja ya sukari, ni aibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi niombe Wizara ya Kilimo ije na mkakati mzuri. Siku moja Mheshimiwa Waziri Mkuu alitembelea katika Mkoa wetu wa Ruvuma, alizungumzia suala hili la kuongeza thamani kwenye zao la mahindi. Akasema kwamba ataangalia namna ya Serikali kuweka mkakati ambao utafanya zao hili la mahindi kuuzwa katika mtindo wa minada kama ilivyo korosho na mazao mengine ambayo kimsingi yamekuwa yakileta tija kwa wananchi. Mheshimiwa Waziri Mkuu, anafanya kazi vizuri pamoja na wasaidizi wake hasa huyo anayeongea naye hapo, wanafanya kazi vizuri sana, hebu jaribuni kuona namna ya kuongeza thamani ya zao la mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, sasa naomba niende kwa mawakala wa pembejeo za kilimo. Rais wetu anafanya kazi nzuri na amekuwa akisema kwamba yeye ni Rais wa wanyonge na wasaidizi wake wamekuwa wakisimamia hivyo. Mimi nashangaa sana inakuwaje mawakala hawa wa pembejeo wana miaka minne wanadai pesa zao walizohudumia Serikali katika sekta hii ya kilimo? Mawakala hawa walikwenda kukopa fedha kwenye taasisi za fedha, wakajikusuru na wakaenda kuwekeza kwenye pembejeo za kilimo lakini Serikali haioni umuhimu wa kuwalipa, inasikitisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikijificha kwenye kichaka cha uhakiki miaka minne. Ni kwa nini Serikali haiendi kuwalipa hawa mawakala wa pembejeo? Wapo mawakala ambao wengine walichukua mbolea TFC inaeleweka walikwenda kuchukua kule walichukua kiasi gani lakini wengine wanapoteza maisha yao wakisubiri kupata haki yao, Wizara mmekaa lakini Serikali pia imejificha nyuma ya suala la uhakiki. Ni uhakiki wa aina gani miaka minne, inatia huzuni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshuhudia wakala mmoja nilipokwenda ziara kule analia. Nimekuta pale dukani kwake kuna makampuni manne yote yanamdai na kila kampuni imeleta dalali, inasikitisha na yule bwana ametoka pale. Nitoe tu mfano kwa mawakala wachache ambao mnaweza mkafuatilia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna dada anaitwa Rose Minjingu, nendeni mkafuatilie pale, amekopa na taasisi zinamdai lakini pia kule alikokopa kwenye kampuni mbalimbali mpaka TFC anadaiwa. Imefika mahali amezungukwa na watu wale kama wanne wanadai, kila mmoja kaja na dalali. Pia yupo kijana anaitwa Cosmas Haule, naye pia amezingirwa, imefika mahali ndugu zake wamekaa chini kumshawishi maana alikuwa anataka kuchukua hatua ya kujinyonga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi hii ambayo watu wanatafuta haki zao na inafika mahali wanashindwa kupata haki zao, hivi kwa nini kama hawa watu kweli wameiba wasipelekwe Mahakamani? Haki zao zinapotea, wengine wanapoteza maisha, inatia uchungu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi hii wako watu ambao haki zao zinapotea, tunakwenda wapi? Wale mawakala walipwe pesa zao, wale ambao wamefanya vizuri walipwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyuma yake kunakuwa na suala la uhakiki, uhakiki gani? Mbona tumeona hawa watumishi wamehakikiwa siku mbili suala limekwenda, wenye vyeti feki wamehakikiwa siku mbili wamekwenda, ni kwa nini huku kwenye Wizara ya Kilimo hawalipwi pesa zao hawa mawakala? Siyo vizuri, msiwadhulumu haki yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea kwa uchungu kwa sababu yuko mtu ambaye alikuwa anataka kujinyonga lakini ndugu zake wamekaa wamemshawishi, inatia huzuni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika wale mawakala, wako mawakala saba ambao tayari wameshapoteza maisha, wako Wabunge ambao ni mashahidi hapa kwenye maeneo yao. Mzee wa Makambako yule pale atasema, kuna watu wamekufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siungi mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema mwingi wa utukufu kwa kunipa uzima ili niweze kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Kilimo na Uvuvi.

Pia nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya katika nchi yetu ya Tanzania. Ni ukweli usiopingika kwamba nchi ya Tanzania sasa inakwenda kupaa kiuchumi, kila baada ya wiki moja tunashuhudia uzinduzi wa miradi mbalimbali, hongera sana kwako Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, niwapongeze sana Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Mheshimiwa Luhaga Mpina na Naibu wako. Nitakuwa sijatenda haki kama sijakupongeza sana Spika kwa namna ambavyo unachapa kazi, kwa namna ambavyo unasimamia Bunge hili, sasa hivi Bunge limetulia, ukiona chombo kimetulia basi ujue kwamba msimamizi wa chombo hicho yuko makini na mambo yanakwenda bara bara, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la uvuvi wa samaki kwa maana ya sekta ya uvuvi. Katika sekta ya uvuvi nitajikita moja kwa moja Ziwa Nyasa. Nimesoma katika hotuba hii ya Waziri wa Mifugo, hotuba yake katika ukurasa wa 82 na 83 kwenye kipengele kila cha utafiti inaonesha kwamba katika utafiti ambao wameufanya katika maziwa yote pamoja na bahari kuna samaki tani 2,736,247 na mchanganuo wake ni kama ifuatavyo; Ziwa Victoria lina tani 2,148,248; Ziwa Tanganyika tani 295,000; Ziwa Nyasa tani 168,000 na Bahari ya Hindi tani 100,000.

Mheshimiwa Spika, katika utafiti huu ambao wameufanya naomba niende kwenye Ziwa Nyasa. Ziwa Nyasa inaoneshwa kwamba pana tani 168,000 lakini naomba nimuambie Mheshimiwa Waziri kwa maana ya utafiti huo naona kwamba tani hizi ni chache. Je, Serikali au Wizara ina mpango gani wa kuinua au wa kuweka mikakati ambayo itaweka uzalishaji mzuri kwenye hilo ziwa ili ziwa hili liweze kuweka samaki wengi zaidi, ukizingatia kwamba Ziwa Nyasa ni ziwa la pili kwa wingi wa maji, kwa hiyo lina uwezo mkubwa sana wa kuweza kutunza samaki wengi.

Mheshimiwa Spika, pia jirani zetu wa nchi ya Malawi wamekuwa wakifanya uhifadhi wa samaki kwa maana ya fish cage, kwa hiyo kwa uzalishaji na utunzaji huo wa samaki umepelekea samaki wetu kutoka huku upande wa Tanzania wanakimbilia kule kwa ajili ya kwenda kupata chakula, kwa hiyo inaonekana kwamba kwenye Ziwa Nyasa upande wa Tanzania hatuna samaki wengi.

Ninaiomba Serikali yangu ifanye mkakati wa maksudi na ninaamini kabisa Wizara hii ina Mawaziri vijana ambao tumeona wanafanya kazi na wanakwenda maeneo mbalimbali. Ninaamini kabisa wana uwezo mkubwa wa kuweka mikakati mizuri ambayo itakwenda kuzalisha na kwa kuwa, namuona Mheshimiwa Mpina amedhamiria kabisa kukuza sekta hii ya uvuvi hebu nenda kafanye utafiti mzuri zaidi na uone namna gani mnaweza kuinua uzalishaji huu katika Ziwa Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mpina toka umepata madaraka haya ya Uwaziri hujaenda kule Ziwa Nyasa ni lini utaenda Ziwa Nyasa ukatembelee ukaone namna ambavyo ziwa lile lilivyo na ni ziwa ambalo lina vivutio vizuri sana vya utalii, kuna samaki wengi wa mapambo, kuna dagaa wazuri watamu kweli na siku moja hapa nilimtolea mfano dada yangu Mheshimiwa Jenista nikasema angalia hiyo brand ya Mheshimiwa Jenista namna alivyokuwa mzuri ni kwa sababu ya samaki wazuri watamu ambao wanatoka Ziwa Nyasa. Lakini pia nenda kamuangalie dada yangu Mheshimiwa Manyanya muda wote yuko vizuri kwa sababu ya samaki wazuri na mimi mwenyewe je?(Kicheko)

Mheshimiwa Spika, karibu sana Mkoa wa Ruvuma katika Ziwa Nyasa uone aina ya samaki watamu na wazuri ambao wana virutubisho vizuri na ukishakula wale samaki hata magonjwa yanakaa mbali.

Mheshimiwa Spika, napata shida sana, nilidhani kwamba unapokuwa na Bahari ya Hindi maana yake kwa ukubwa wake tunaweza tukawa tunapata tani nyingi za samaki kule, kumbe hii methali inayosema ukubwa wa pua siyo wingi wa..., samahani. Nashangazwa na tani chache hizi ambazo zimeainishwa hapa kwa maana ya utafiti uliofanyika kwenye Bahari ya Hindi. Wizara mna mkakati gani wa kuweka mpango mzuri ambao utakwenda kuhakikisha kwamba Bahari ya Hindi tunaitumia vizuri ili tuweze kupata pato kubwa.

Mimi siyo mtaalam wa mambo ya uvuvi lakini naona niongelee, halafu ninyi kama Wizara mtaona namna ya kuweka vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia Wizara iwezeshwe kwa pesa, kama tunazungumzia kwamba waweze kuinua uchumi, waweze kufanya mambo mbalimbali kwenye sekta hii, basi tuhakikishe kwamba hii Wizara inapewa pesa ili iweze kutekeleza majukumu yote ambayo tunadhani kwamba yanafaa kwa Wizara hiyo.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho naomba nirudie tena kumshukuru sana Mheshimiwa Rais aendelee kufanya kazi na kwamba wenzetu sasa Wapinzani wetu wamekuwa kama vile wamepanda basi ambalo wanaendesha gizani na wanatembelea taa za parking, Mheshimiwa Rais endelea kuchapa kazi, tuko nyuma yako, tunakuunga mkono sana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, mwingi wa utukufu aliyenijalia kusimama hapa siku hii ya leo. Pili, nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye taarifa za utekelezaji wa shughuli za Kamati za Bunge za mwaka 2018/2019 ambazo ni Kamati za Maendeleo ya Jamii, Serikali za Mitaa na UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba niende kwenye suala linalohusu maboma. Katika maboma ambayo yamejengwa na wananchi kwenye suala la afya na elimu ikiwa ni madarasa pamoja na zahanati na vituo vya afya ni mengi sana katika nchi hii. Inapotokea kwamba nguvu za wananchi ambazo zimetumika, wananchi ambao wamejitolea kwa dhati kabisa kujenga maboma yale na ikaonekana kwamba nguvu za wananchi hawa zinapotea bure wananchi hawawezi kuielewa kabisa Serikali dhidi ya nguvu zao ambazo zinapotea bure. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie namna ya kuweka mkakati wa makusudi kabisa kuhakikisha kwamba maboma yale yanamaliziwa na watoto wetu waweze kuanza kuyatumia kwa madarasa lakini pia zahanati na vituo vya afya vianze kutumika haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la Local Government Development Grant. Huu mfuko ulikuwa unasaidia sana Halmashauri zetu, najiuliza ni kwa nini Serikali imeondoa Mfuko huu? Kama kulikuwa na changamoto zozote kwa nini Serikali isi-maintain Mfuko huu ili mwisho wa siku uweze kuendelea kusaidia katika Halmashauri zetu?

Mheshimiwa Spika, kuna suala linahusu TARURA. TARURA ni jambo ambalo limeletwa kama ugatuaji wa madaraka katika Serikali za Mitaa. Hata hivyo, TARURA huyu yeye ni kama wakala tu katika Halmashauri hizo kwa sababu barabara ni Halmashauri lakini pia hata fedha ni za Halmashauri. Mimi nashangaa sana huyu TARURA anaposhindwa kuwa ni miongoni mwa wajumbe ambao wanashiriki kwenye vikao vya Mabaraza ya Halmashauri zetu ili wale Madiwani waweze kusema ni barabara ipi ambayo inatakiwa itengenezwe badala ya TARURA wao kukaa tu kama kakikundi pembeni wakaanza kujipangia wenyewe kwamba tunakwenda kutengeneza barabara hii, barabara hii bila kujali kipaumbele cha wananchi ambao wanawakilishwa na Madiwani ambao wanajua kipaumbele cha barabara za kutengenezwa.

Mheshimiwa Spika, nilidhani kwamba utaratibu huu ungerekebishwa. Nitole tu mfano, anakuja mtu anaingia nyumbani kwako, anaanza kuchukua sufuria jikoni, anakwenda chumbani kupika, anavuruga utaratibu. Kwa hiyo, ni vizuri hawa TARURA wakashirikishana na wakawa
wanaripoti kwa Halmashauri ili waweze kubainisha vizuri zile barabara na taratibu zote ziweze kwenda sawia. Nachoamini ni kwamba Diwani wa Halmashauri au Halmashauri haitakuwa na mamlaka ya kupanga au kutafuta wazabuni lakini hata kuelekeza tu kwamba nadhani barabara hii kutoka sehemu fulani mpaka sehemu fulani ingefaa itengenezwe kwa sasa kulingana na changamoto iliyopo, nayo pia wananyimwa? Ni jambo gumu sana.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niende kwenye suala la watumishi wa Halmashauri. Kwenye suala la afya na elimu kuna changamoto ya watumishi hasa hapa kwenye suala la afya. Zahanati zetu unakuta labda kuna Daktari mmoja au sehemu nyingine hakuna Daktari kabisa ni Mhudumu tu wa kawaida kama Nesi anafanya kazi za udaktari, huyo huyo azalishe na shughuli nyingine, kwa hiyo, kumekuwa na shida kubwa sana. Utendaji kwenye zahanati zetu na vituo vya afya hauridhishi mwisho wa siku tutaendelea kuwaumiza wananchi wetu, watakuwa hawapati matibabu yale yanayostahili kulingana na vile ambavyo ingefaa.

Mheshimiwa Spoika, sasa naomba niende kwenye suala la UKIMWI, naomba hapa mnisikilize kwa makini sana. Tanzania 90, 90, 90 inawezekana lakini inawezekana pale tu ambapo kutakuwa na ruhusa ya watu kujipima wenyewe. Kuna watu wengine wanaona aibu kwenda kupimwa kwenye vituo vya upimaji hasa wanaume. Hawa ndiyo wamekuwa wakifanya kazi ya kusema kwamba maadamu wewe umepima basi tutakuwa tuko sawa, siyo kweli. Ni kwa sababu tu wanaona aibu kwenda kupima lakini utaratibu wa kila mtu kujipima mwenyewe utakuwa ni mzuri zaidi, mnaweza mkakaa watu wawili wenyewe mkajipima, ukampima mwenzako na wewe ukampima mkapata majibu hapo hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika suala la UKIMWI kuna suala la mkono sweta. Mkono sweta kwa utafiti ambao umefanyika…

SPIKA: Mheshimiwa Jaqcueline, Kiswahili hiki sijui kama kila mtu anelewa ni kitu gani hicho. (Kicheko)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, mkono sweta ni wale wanaume ambao hawajatahiriwa. Hili jina wamejaribu kuliboresha sana badala ya kuliita govi wamesema mkono sweta angalau limeboreshwa boreshwa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mkono sweta ni janga.

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nimeipokea kwa mikono miwili na nashauri tuanze na Wabunge wote humu ndani ambao pengine watabainika hawajafanya hiyo tohara basi wafanyiwe mara moja. (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Bahati mbaya hoja yako haikuungwa mkono. Endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, naomba nilindie dakika zangu.

Mheshimiwa spika, suala la mkono sweta ni tatizo kubwa. Ili kufikia 90, 90, 90 ni lazima tuhakikishe kwamba mikono sweta yote inaondolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utafiti uliofanyika unaonyesha kwamba mkono sweta umekuwa ukiambukiza magonjwa mbalimbali ikiwa ni pamoja na ugonjwa wa UKIMWI. Maambukizi ni kwa mwenye mkono sweta lakini pia kwa mwanamke kwa asilimia 60. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda niseme ni namna gani ambavyo unaambukiza UKIMWI lakini pia umekuwa ukiambukiza kansa. Endapo mkono sweta ule umekutwa na virusi aina ya human papilloma virus ni rahisi kumuambukiza mwanamke virusi hivyo ambavyo mwisho wa siku mwanamke anakuwa anapata kansa ya kizazi. Kwa hiyo, naomba sana…

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, kwa kweli sasa naongea kwa masikitiko sana. Pale unapoona kwamba hawa wanaume wenye mikono sweta wanakwenda kuwaambukiza wanawake wenzetu ikiwemo pengine na wanawake wengine kama itatokea…
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kuchukua nafasi hii kuchangia Wizara ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo la ardhi ya wananchi ambao wametoa ardhi yao kwa EPZ ambao wamechukua eneo la Kata ya Mwengemshindo katika Manispaa ya Songea, lakini wananchi hao hawajalipwa fedha zao za fidia mpaka sasa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha wananchi hawa ambao wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu bila kulipwa fedha, walipwe ili waweze kuendeleza shughuli zao?

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Usindikaji wa Tumbaku (SONAMCU) kilichopo katika Manispaa ya Songea, mwaka jana mwezi Mei niliuliza ni lini Kiwanda cha SONAMCU kitaanza, majibu yalikuwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshapata mwekezaji ambaye tayari ameshasaini mkataba wa kuendesha kiwanda hicho na kwamba kiwanda hicho kitaanza kufanya kazi Mwezi Agosti, 2018, lakini mpaka sasa kiwanda hiki hakijaanza; tatizo ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, tangawizi; katika Wilaya ya Songea Vijijini katika Kata ya Mkongotema, Wino, Madaba na Maweso wanalima sana zao la tangawizi ambalo limekuwa linatumika kama chakula, dawa na kadhalika. Kwa kuwa zao hili ni muhimu sana na linazalishwa kwa wingi katika maeneo niliyoyataja, Wizara hii ingetafuta namna ya kufanya au kuwasaidia wakulima hao kupata wawekezaji wa kiwanda ili waweze kuongeza thamani ya zao hili na tija kwa maisha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara iangalie namna ya kuwawezesha wakulima wa zao la mahindi kwa kutafuta wawekezaji wa viwanda vya uchakataji wa zao la mahindi. Ni matumaini yangu kuwa Wizara ikijipanga vizuri haya yote yanawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mchango wangu huu wote uingie kwenye Hansard.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza Wizara ya Kilimo kwa kazi nzuri sana, wanayoifanya ya kusimamia na kutekeleza majukumu waliyopewa.

Mheshimiwa Spika, Zao la mahindi, halijapewa kipaumbele licha ya kuwa Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa mikoa mikubwa minne inayozalisha mahindi kwa wingi sana na zao hili bado halijawekewa mkakati madhubuti wa soko na mbegu bora.

Mheshimiwa Spika, je, Wizara ina mpango gani wa kufanya utafiti wa mbegu bora ambazo zitaleta tija kwa mkulima kulingana na aina ya mbegu na udongo unaostahili kulimwa mahindi, na utafiti huo utachukua muda gani ili kuharakisha utekelezaji huo ili kuokoa nguvu za wakulima zinazopotea bure kwa uzalishaji usio na tija?

Mheshimiwa Spika, zao la tangawizi linalimwa sana katika Wilaya ya Songea Vijijini katika Halmashauri ya Madaba maeneo ya Mkongotema, Mahanje, Madaba, Wino na maeneo mengine. Tangawizi ni chakula, tangawizi ni dawa na imekuwa ikitumika sana katika mapishi mbalimbali. Je, Serikali ina mpango gani katika kuwekeza zao hili ambalo limekuwa linakuza uchumi katika nchi yetu ya Tanzania?

Mheshimiwa Spika, lakini, pia limekuwa likiuzwa ndani ya nchi yetu tu ilhali ziko nchi mbalimbali ambao wamekuwa wakitumia tangawizi kama chakula na dawa. Ninaomba Serikali ilete wataalamu katika maeneo yaliyotajwa hapo juu ili kuendelea kutoa elimu elekezi kwa wananchi. Ni imani yangu kuwa kwa kufanya hivyo itasaidia sana kuongeza tija katika uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, Masoko, soko la mahindi ni tatizo kubwa sana, ningependa Serikali itafute soko la uhakika la mahindi. Halikadhalika ninaomba Serikali itafute soko la tangawizi, mbaazi, mahindi na mazao mengine.

Mheshimiwa Spika, mwisho, Mawakala wa Pembejeo. Mawakala wa pembejeo hawajalipwa pesa zao kwa muda mrefu sana. Je, tatizo ni nini? Siku zote majibu ya Wizara ya Kilimo na Wizara ya Fedha ni juu ya suala la uhakiki, je uhakiki huo utaisha lini? Mimi sioni kama mawakala wote walifanya udanganyifu kwa Serikali bali ninaamini kuwa kati yao wapo waliofanya vizuri. Sasa ni kwa nini hao waliofanya vizuri wasilipwe? Ninachelea kusema kuwa Serikali haiwatendei haki mawakala wa pembejeo, ninaomba mchango wangu Hansard.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, mwingi wa utukufu kwa kunipa uzima ili nami niweze kusimama hapa leo kuweza kuchangia Kamati zote tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na suala la utawala bora. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli; nampongeza Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan; nampongeza Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa kwa utendaji mzuri wa kazi unaozingatia suala la utawala bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utekelezaji wa majukumu ya Rais tangu amekuwa Rais toka mwaka 2015, pamoja na kazi nyingi sana alizozifanya za kuhakikisha kwamba Tanzania yetu inaendelea kupaa kiuchumi, leo hii nitataja baadhi tu ya mambo ambayo ameyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kusimamia kwa makini kabisa suala la rushwa; matumizi mabaya ya fedha na rasilimali za Taifa; amesimamia suala la kuondoa watumishi hewa; na ametoa elimu bure. Mpaka sasa tangu elimu bure imeanza kutolewa ni fedha zaidi ya shilingi trilioni moja ambazo zimetumika. Hongera sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuimarisha mikopo ya elimu ya juu. Hakuna malalamiko wala maandamano. Ahsante sana Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais amesimamia ujenzi wa Stiegler’s Gorge; zaidi ya pesa trilioni sita zimetolewa; amesimamia vizuri miradi ya maji inayoendelea kutekelezwa katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu; amesimamia suala la Vituo vya Afya kuhakikisha kwamba anatoa fedha vituo 352 vinajengwa; ndege nane zinanunuliwa; hospitali 67 mpya; na hospitali za mikoa tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameendelea kutekeleza majukumu yake. Amekubalika ndani ya nchi, nje ya nchi na Bara zima la Afrika. Ndiyo maana amepata nafasi ya kuwa Mwenyekiti wa Nchi zote 16 za SADC. Tuna kila sababu ya kumpongeza Rais wetu. Haya ni baadhi tu ya mambo machache ambayo Mheshimiwa Rais amefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia suala la utawala bora, sijakusudia kuchoma sindano lakini kwa sababu nasikia sauti za wanawake wenzangu wanachoma choma sasa naenda kuchoma sindano. Tunapozungumzia suala la utawala bora ni vizuri pia tukaangalia hata kwenye vyama vyetu, hali ikoje? Kweli tuko kwenye misingi ya utawala bora au tunapiga kelele tu kwa upande wa pili wakati sisi wenyewe hatuko vizuri kwenye suala la utawala bora?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakwenda kwenye Chama ambacho ni cha Demokrasia na Maendeleo. Chama hiki ukiangalia katika uchaguzi uliopita…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Tulieni mpate elimu kidogo. Katika uchaguzi uliopita, viongozi wote waandamizi wa chama hicho wamewekwa kwa maana ya udini; ni Wakristo watupu. Pia, ukienda katika hoja hiyo hiyo, ukiangalia katika Kanda ya Arusha kuna bwana mmoja anaitwa Ali Bananga…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa. Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …aligombea nafasi na akaenguliwa. Huo ni ubaguzi wa hali ya juu. Pia ukienda…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …kwa Mheshimiwa Sumaye, alifanyiwa kampeni ya kupigiwa kura za hapana. Huo ni ubaguzi wa hali ya juu sana. Vile vile ukienda kwa suala la Mheshimiwa Joseph Selasini aliondolewa kwenye nafasi ya Chief Whip kimtindomtindo tu…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Sasa suala la utawala bora hapa likoje? Tunapozungumzia suala la utawala bora, suala la utawala bora likoje?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mwongozo wa Spika.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii...

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mwongozo wa Spika.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kusema kwamba tunapozungumzia suala la utawala bora katika huko huko…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mwongozo wa Spika.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …upande huo huo wanaopiga kelele kuna ndoa za jinsia moja. Sasa unapozungumzia…

MBUNGE FULANI: Choma sindano, choma sindano.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MBUNGE FULANI: Mwongozo wa Spika.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Au unapofanya vitendo vya ndoa ya jinsia moja…

MBUNGE FULANI: Rudia hiyo ya jinsia moja hiyo!

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sehemu ya utawala bora?

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hatujaskia hiyo ya ndoa. hiyo ya ndoa hiyo!

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Hii sio sehemu ya utawala bora…

MBUNGE FULANI: Mwongozo wa Spika.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Ndoa za jinsia moja upande huo siyo sehemu ya maadili. Siyo sehemu ya utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi za Afrika…

MBUNGE FULANI: Mwongozo wa Spika.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi za Afrika, Tanzania imetajwa kwamba ni nchi ambayo inathamini na kujali suala la utawala bora. Imeshika nafasi ya juu kabisa…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwongozo.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …na ndiyo maana wamejitokeza baadhi ya wanasiasa wanakwenda kuropokaropoka hata nje ya nchi, akiwepo Mheshimiwa Zitto Kabwe, akiwepo Mheshimiwa Tundu Lissu na wengine wengi. Akina Mheshimiwa Lema hawa.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie suala la TRA.

MBUNGE FULANI: Mwenyekiti una double standards.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Naomba nizungumzie suala la TRA.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jacqueline, malizia dakika moja.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia. tunapozungumzia suala la utawala bora tujiangalie na sisi.

MBUNGE FULANI: Majambazi wako kule, akina Lema.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Majambazi wako upande huo! Ndoa za jinsia moja ziko upande huo! Hii siyo sehemu ya utawala bora. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji) MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Jacqueline, umemaliza muda wako.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana; kwanza naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapambano dhidi ya uvuvi haramu; nichukue nafasi hii kuipongeza sana Wizara, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, Naibu Waziri na delegation yake yote, hongereni sana kwa kazi nzuri ya mapambano dhidi ya uvuvi haramu. Mapambano haya yameleta tija sana katika nchi yetu lakini pia niwapongeze sana kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato, asilimia 150 haijapata kutokea, hongereni sana. Wizara ina vijana makini wanafanya kazi kwa weledi na ndiyo maana Wizara inaoneka sasa ina uchechemuzi, mambo yanaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika tano ni chache sana lakini naomba kwa ruhusa yako utaniongeze kidogo ili niweze kumalizia. Niwashauri sasa Mheshimiwa Waziri na delegation yake, wazingatie sana ushauri ambao Waheshimiwa Wabunge wanautoa humu ndani dhidi ya mapambano ya uvuvi haramu. Ushauri huu utawasaidia sana kuboresha na kuongeza tija katika Sekta hii ya Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye Ziwa Nyasa; kupitia suala la uvuvi haramu kwa maana ya ushauri ambao nataka kuutoa. Uvuvi haramu pia umeathiri sana katika Ziwa Nyasa, ndugu zetu wavuvi katika Ziwa Nyasa wamepata shida kwenye suala la nyavu, nao pia wamechomewa nyavu. Kwa hiyo, niombe wale wavuvi wamechomewa nyavu kupitia zao la samaki, lakini pia zao mahsusi sana la samaki anaitwa kituhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituhi ni samaki mdogo sana, mtamu na mwenye virutubisho vingi sana, lakini huyu kituhi kwa umbile lake ni mdogo, ndivyo alivyo. Ni sawasawa na binadamu na sisi nao tuna maumbile tofauti tofauti, huwezi kwamba huyu ni mfupi, basi ni mdogo basi siyo binadamu kamili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka niseme samaki anayeitwa kituhi ni mfupi anafikia inchi karibu mbili au tatu. Kwa hiyo, sasa imekuwa ni shida, wavuvi wemechomewa nyavu na kwamba samaki huyu hawezi kuvuliwa. Sasa nataka niseme hivi Mheshimiwa Waziri kwamba naomba atambue wazi kwamba yule samaki hivyo alivyo ndivyo alivyo, kwa hiyo, naomba arudi Ziwa Nyasa akafanye mambo ambayo yatakuwa yanaleta uzalishaji wenye tija katika Ziwa Nyasa. Pia kutokumvua huyu samaki maana yake Mheshimiwa Waziri na delegation yake wanataka sisi Wangoni tuwe wadumavu. Samaki huyu anatusaidia sana kutustawisha kama mnavyotuona katika Bunge hili tumestawi na tumenawiri barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la josho katika Kata ya Linga, naomba Mheshimiwa Waziri atume watu wake kule katika Kata ya Linga kuna wafugaji wengi lakini hakuna josho, tunataka...

MWENYEKITI: Nimekuongezea dakika mbili.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba pia tupate mabwawa ya ufugaji wa samaki. Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake, kule Ruvuma kuna mama zao na vijana wenzao, wanahitaji kuwekeza kwenye mabwawa ya samaki. Tunawaomba sana waje wafanye uwekezaji kule wawasaidie ili waweze kufanya uwekezaji kwenye mabwawa ya samaki. Pia, walete ng’ombe na sisi tunahitaji kufuga, walete ng’ombe sisi tutawasimamia na umeme sasa hivi wa gridi upo, hivyo tunahitaji kuweka viwanda ili tufanye uchakataji kwenye viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa ziara yake aliyoifanya Mkoani Tanga kwenye Kiwanda cha Tanga Fresh. Alipofika kule alikuta kuna changamoto kubwa sana ambayo ilikuwa ni kikwazo kikubwa sana cha kukuza uzalishaji katika kiwanda kile hasa kwenye uzalishaji wa maziwa ambayo ni UHT, haya maziwa ni mazuri lakini pia yana uwezo wa kutunzika kwa muda mrefu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais alichokifanya alikwenda kuondoa changamoto ya suala la ardhi kwenye kiwanda hicho, akatoa maelekezo ardhi ile wakaipata na wakaenda kukopa wakapata bilioni 10. Sasa hivi wamefanya uwekezaji mzuri na leo kila Mbunge hapa alishika kamfuko amepata maziwa, Magufuli oyee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakwenda kwenye Kiwanda cha Asas, nao pia niwapongeze sana kwa uzalishaji mzuri sana wa maziwa ya UHT. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Wizara kwa kusimamia kuhakikisha kwamba kunakuwa na viwanda vya uchakataji wa nyama; Kiwanda cha Kibaha na Longido, hongera sana wako vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niseme hivi, nawapongeza tena kwa kuhakikisha kwamba wanaweka mkataba kati yao na nchi ya Misri, Misri wanakuja kuchakata hapa nyama lakini pia Misri wanakuja kuwekeza kwenye ngozi, tutapata ngozi zetu lakini pia tutaweza kutengeneza mikoba, mikanda na mambo mengine… (Makofi)

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu…

MWENYEKITI: Ahsante sana, Mheshimiwa Jacqueline.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wenzetu Ethiopia wameweza…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …kama wenzetu Ethiopia wameweza, sisi tunashindwaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya nakushukuru sana, naomba…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Jacqueline.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ametushtua anasema UTI, kuhusu utaratibu.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nani kama Dkt. John Joseph Pombe Magufuli. Waheshimiwa Mawaziri oyeee. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Niende moja kwa moja kwenye hoja zangu za msingi. Hoja ya kwanza inahusu suala la utalii. Nichukue nafasi hii kuipongeza sana Wizara kwa kazi nzuri ya ubunifu ambayo inaifanya; mpaka sasa tunaona kwamba watalii wamekuwa wakija kwa wingi kutoka nchi mbalimbali; Israel, Malaysia, China na maeneo mengine, hongera sana kwa vijana ambao wanafanya kazi katika Wizara hii na siku moja Mheshimiwa Dkt. Kigwangwala alisimama hapa akasema yeye si wa mchezo mchezo; hii imejidhihirisha wazi katika utekelezaji majukumu yao ambayo wanayafanya pamoja na Naibu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujua kwamba huu Mradi wa Utalii katika Mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma ni lini utapelekwa na unapita kwenye maeneo gani? Nataka kusema kwamba kule tuna Selous Game Reserve, tuna Liparamba, tuna Makumbusho ya Majimaji, lakini tuna zoo moja ya Ruhira pale ni zuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile pale Njombe tuna nyumbanitu, nyumbanitu ni maeneo ambayo yana vitu vya ajabu ajabu sana. Kuna kuku wapo mle wanaishi kwenye ule msitu hajulikana nani amewafuga na wapo humu wakiwa na rangi nyeusi. Pia wapo ng’ombe wanazunguka kwenye hilo eneo, hajulikani nani amewaweka, kwa hiyo ni nzuri sana watalii wakienda kwenye maeneo haya yakiwemo pamoja na maeneo hayo ya Mkoa wetu wa Ruvuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie Mto Ruvuma; mto huu umekuwa na mamba wengi sana ambao wamekuwa wakileta athari kubwa sana kwa wananchi wa Mkoa wa Ruvuma. Niwaombe Wizara ije iwavune hawa mamba, lakini pia siku moja nilimsikia Mheshimiwa Mulugo alizungumza hapa kuhusu Ziwa Rukwa napo kumekuwa na mamba wengi sana. Wizara ifanye juhudi za makusudi kuwavuna hawa mamba ili wasiendelee kuleta athari.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukurasa wa tatu kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake, aya ya tatu lakini pale imeandikwa namba tisa, naomba niseme suala ambalo kimsingi linatia huzuni, lakini pia tumekuwa tukiwazungumzia sana ndugu zetu ambao wamekuwa wakiathirika na masuala hasa yanayozunguka kwenye maeneo ya wanyamapori. Tumekuwa tukisahau kuwazungumzia askari wetu ambao ndio wanasimamia na kulinda rasilimali hii ya Tanzania. Askari hawa wamekuwa wakijeruhiwa, wangine wamekuwa wakichomwa na mishale ya sumu, wengine wamekuwa wakujeruhiwa na hawa majangili, wamepoteza maisha, nimeona kwenye hii aya wapo zaidi ya 11.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana, hawa vijana wamejitoa wengine wanaumwa na nyoka, wanalala huko porini tuwatie moyo. Niombe sana Wizara hii, kwanza niwape pole kwa kupoteza hao vijana, lakini pia niombe stahili zao wanazostahili wapewe. Ikiwezekana waongezewe hata kiwango cha mshahara ili waweze kufanya kazi vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala ambalo Mheshimiwa Waziri amesema kwamba anatupa offer. Mheshimiwa Waziri tunakushuru sana kwa hii offer ya futari. Hata hivyo, niombe amekuwa akitupa futari kila wakati tunamshuru sana, lakini safari hii afanye kitu kingine mbadala, atualike Bunge zima kwenda kufanya utalii katika Mbuga ya Ngorongoro, Serengeti, Saadani na maeneo mengine, futari tumekula sana baba.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Mawaziri wanafanya kazi nzuri sana, waendelee kuchapa kazi. Matarajio ya Mheshimiwa Dkt. John Joseph Magufuli anayoyatarajia kufikia mwaka 2020/2025 ni makubwa na wao ndio vijana amewaweka na amewaamini, waendelee kuchapa kazi. Kazi zao ni nzuri, wanasikiliza watu vizuri, wanatoa maelekezo vizuri, tunawashukuru hawajidai wala nini. Pia Makatibu Wakuu, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu wapo vizuri, nimekwenda ofisini kwa Katibu Mkuu amenisikiliza vizuri na tatizo langu likatatuliwa kwa haraka, nashukuru sana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, naanza kwanza kwa kukupongeza wewe uliyenipa nafasi hii ya kuchangia. Wewe ni Spika wa kiwango cha hali ya juu, lakini pia mwenye weledi, mwadilifu, mwenye busara na ni mchapakazi. Nakupongeza kwa dhati hasa kwa sababu ya utendaji wako mzuri wa kazi, lakini pia kwa ajili ya Bunge mtandao.

Mheshimiwa Spika, mimi binafsi imenisaidia sana. Kwanza imenisaidia kuongeza uelewa, lakini pia imenisaidia kuondoa mabegi na viroba vya vitabu ambavyo vilikuwa vinajazana nyumbani kwangu. Ahsante sana. Sasa hivi nyumba imekuwa na nafasi ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wangu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais anayetokana na Chama cha Mapinduzi, Chama ambacho kina sera nzuri, chama imara, kinakubalika na sera zake zinatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nawapongeza wasaidizi wake, Makamu wa Rais pamoja na Waziri Mkuu. Waziri mkuu amekuwa akifanya kazi nzuri sana. Tumemwona kila maeneo ya nchi yetu. Kama kuna jambo lolote linajitokeza, basi mara moja anatokea na kuweza kufanya suluhisho la jambo hilo ambalo liejitokeza. Hongera sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mungu akujaalie kila la kheri, akupe uzima na afya njema na Bunge lijalo urudi ukapate kura za kishindo, ikiwezekana upite bila kupingwa Ruangwa. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina kila sababu ya kuendelea kupongeza Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo anasaidiwa na wanawake wawili mahiri sana; Mheshimiwa Jenista Joachim Mhagama na Waziri Angellah Kairuki. Hawa akina mama wanafanya kazi vizuri sana.

Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria ambaye ninafanya kazi sana na Ofisi ya Waziri Mkuu. Tunaona namna ambavyo wamekuwa wakijibu hoja zetu Waheshimiwa Wabunge ambao ni Wanakamati na pia tumeona umahiri wa utendaji wao wa kazi. Hongereni sana, wanawake, tunaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa misingi hiyo ndiyo maana wameweza kukidhi maono ya Mheshimiwa Rais; kwanza kwa uratibu mzuri ambao wamekuwa wakiufanya na usimamizi mzuri. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, progaramu ya kukuza ujuzi kwa vijana ambayo iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, imetekelezwa vizuri sana. Kutokana na ufinyu wa ajira, lakini Wizara hii imekwenda mbali zaidi, vijana wengi wameweza kupelekwa kwenye mafunzo ya Vyuo vya Ufundi Stadi ikiwepo VETA na vyuo vingine kama Don Bosco. Vijana wamepata mafunzo mazuri sana.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tunapozungumzia suala la ajira kwa vijana huwezi kuacha kuzungumzia suala la vitalu nyumba ambayo inaitwa greenhouse, ambapo kwa mapana na marefu sana sisi tumekwenda tumekagua miradi mbalimbali ya vijana kwenye kila Halmashauri, miradi hii imewekwa. Niseme tu baada ya muda mfupi, inawezekana kabisa tukawa tumefikia uchumi wa kati tunaoutarajia kupitia hawa vijana. Vijana hawa pia wamejikita katika shughuli za viwanda vidogo vidogo vya utengenezaji wa chaki, pamoja na kutengeneza mafuta na mambo mengine mengi. Kwa kweli Ofisi hii iko makini sana.

Mheshimiwa Spika, miradi mikubwa ambayo inaendeshwa katika nchi yetu inayotekelezwa kwa sasa ikiwemo miradi ya barabara za lami lakini pia reli ya umeme, standard gauge, Stiegler’s Gorge, bomba la mafuta, umeme wa REA na usafiri wa anga, kwa kweli imeleta tija sana katika nchi yetu. Miradi hii imefungamanisha maendeleo ya watu, uchumi wa nchi pamoja na kipato cha kila mmoja. Miradi hii imeongeza ajira. Uchumi wa sekta binafsi kwa kutoa huduma umekua.

Mheshimiwa Spika, miradi hii pia imesababisha wananchi kupata kipato kupitia katika shughuli mbalimbali, mfano; kwenye suala la ujenzi, wananchi waweza kupeleka kokoto, wameweza kuuza cement, kukusanya mchanga na kupeleka maeneo ya ujenzi. Kwa hiyo, hii imesaidia sana kukuza kipato kutokana na miradi hiyo mikubwa.

Mheshimiwa Spika, nachelea kusema miradi hii ina tija na niseme tu kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu iendelee kutoa mafunzo mbalimbali ili hawa vijana waweze kuendelea kuwekeza na kupata tija zaidi katiak maisha yao.

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Tume ya Uchaguzi kwa sababu imetekeleza takwa la kikatiba na kisheria kwa kuboresha daftari la kudumu. Hata sasa tunavyozungumza wananchi wapya zaidi ya milioni saba wameweza kujiandikisha katika daftari la kudumu. Sasa niseme tu, kwa wale wenzetu wenye tabia ya kuchukua mpira na kuweka kwapani, safari hii tunaomba sana msichukue mpira kuweka kwapani na kukimbia uwanjani. Twendeni uwanjani, uchaguzi upo, twende tukapambane uwanjani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Kamishna Mkuu wa TRA, Dkt. Mhede, kwa kazi nzuri sana ambayo anaifanya ya ukusanyaji wa mapato. Amekuwa mbunifu na tumeshuhudia mwezi Desemba amekusanya mapato na kufikia shilingi trilioni 1.9, haijapata kutokea. Pongezi nyingi sana kwake. Namwomba tu Rais wangu kipenzi, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, ikibidi huyu Dkt. Mhede ampe zawadi nono.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia suala la kukua kwa maendeleo, ni muhimu sana tukazungumzia pia barabara ambazo ziko pembezoni kwenye mikoa ya pembezoni ili kuweza kufungua mawasiliano ya kiuchumi na uchumi wetu uweze kukua kwa pamoja, usiende kukua kwa upande upande. Kwa mfano hapa, nitazungumzia barabara ambayo ina urefu wa kilometa 124, inayotoka Songea Mjini kwenda Mkenda. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Jacqueline.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JAQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema na Mwingi wa Utukufu aliyeniwezesha kusimama hapa leo. Jambo la pili niwashukuru sana wanawake wa Mkoa wa Ruvuma ambao walinipa kura nyingi sana za kishindo zilizonisababisha mimi kuingia ndani ya Bunge na kuwa Mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikishukuru chama changu cha Mapinduzi, lakini pia niishukuru familia yangu. Nasema ahsante sana wote walioshiriki kuniwezesha, Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, lakini pia Mpango wa Maendeleo wa Mwaka Mmoja. Ili tuweze kujenga uchumi ni lazima tushirikishe uchumi wa viwanda pamoja na masuala mazima ya kilimo, bila kuhusianisha hivi vitu hatuwezi kufika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa viwanda unategemea sana sekta ya kilimo kwa asilimia 80. Kwa hiyo, vyovyote vile iwavyo lazima tuweke mkakati wa makusudi kuhakikisha kwamba kwenye eneo la kilimo tunakaa sawasawa. Ni lazima tuhakikishe kwamba pembejeo na zana za kilimo zinapatikana kwa urahisi ili kuweza kufanya mageuzi makubwa sana katika sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maafisa Ugani nao pia kuanzia vitongoji, vijiji, kata, wilaya kwenda mpaka mkoa ni lazima kuhakikisha kwamba wanakuwa ni wale ambao wanaweza kwenda mpaka chini na kutoa mafunzo mazuri kuhusiana na masuala ya kilimo ili wananchi wetu waweze kufanya uwekezaji wa kilimo wenye tija. Badala ya hivi ilivyo sasa wananchi wanalima kiholela na wala udongo haupimwi kwamba kwa udongo huu sasa mnaweza kulima migomba au pamba, wanalima tu kwa kubahatisha. Kwa hiyo, wataalam wakisimama makini kabisa na wakaweza kupima udongo ni imani yangu kwamba tutatoka hapa tulipo na tutasonga mbele zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo na umwagiliaji. Nilidhani pia kwenye eneo hili tuhakikishe kwamba Serikali inaweka fedha nyingi katika kuandaa miundombinu ambayo itawezesha suala la ulimaji wa umwagiliaji ili wananchi au Tanzania yetu tuweze kuwekeza kwenye kilimo na tuweze kuvuna mara mbili kwa mwaka au zaidi. Hapo ndipo tutakapoweza kuviwezesha viwanda vyetu viweze kufanya kazi na viweze kuzalisha na hatimaye kuleta ajira nyingi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia suala la mbegu lizingatiwe. Nashauri Serikali ione namna gani itaweza kuzalisha mbegu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nizungumzie suala la masoko. Hivi sasa tunazungumza masuala ya kilimo lakini wananchi wanapokuwa wamevuna mazao yao masuala ya masoko ni kubahatisha, hawana masoko ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti,nikizungumza hapa wale ambao wanazalisha mazao ya nafaka katika Nyanda za Juu Kusini ukiangalia zao la mahindi wananchi bado wana mahindi ya mwaka jana na yakakutana na mwaka huu. Kwa hiyo, ni wazi kwamba, mwananchi hapo hawezi kufanya uwekezaji wenye tija na wala hatuwezi kufikia malengo tunayoyatarajia. Kwa hiyo, nilidhani kwenye eneo hilo basi, liwekewe mkakati wa makusudi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Benki ya Kilimo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imegonga Mheshimiwa, ahsante.

MHE. JAQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, umenikatili. Ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, Naibu Spika, ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana nichangie katika Wizara hii hasa kwenye maeneo ya vyuo vikuu. Nataka niiambie Wizara ya Elimu kwamba, kumekuwa na vyuo vikuu ambavyo vinaendeshwa na taasisi za dini nchini Tanzania, lakini taasisi hizi tayari zimeanza kukata tamaa na kwamba, vyuo hivyo sasa hivi vinalegalega, havifanyi vizuri, lakini ninachofahamu ni kwamba, Wizara ya Elimu ndio walezi wa vyuo hivi. Kwa hiyo, ni vizuri sasa Wizara ikasimama katika kuhakikisha kwamba, hawa wanafanya vizuri kwa kuwasaidia resources mbalimbali ikiwemo pesa pamoja na watumishi ambao wanatakiwa wafanye kazi kwenye taasisi hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa hizi taasisi nazo pia zinafanya vizuri katika kuongeza elimu katika nchi yetu na zimekuwa zikifanya vizuri sana. Kwa hiyo, Wizara isimame katika eneo lake na kuhakikisha kwamba, wanawawezesha ili waweze kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa sana imeonesha kwamba, vyuo hivi na taasisi hizi zinaendelea kufa hasa ninapozungumzia chuo kimoja pale Mkoa wa Mtwara. Nacho kimekufa, chuo hakifanyi vizuri na Wizara wapo, wamekaa wanaangalia tu. Pia kuna Chuo cha AJUCO, Songea Mjini, chuo kile kimekufa hakiendelezwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa nikifikiria tu ni kwa nini Mheshimiwa Profesa Ndalichako anajisikiaje Nyanda za Juu Kusini kule vyuo vyetu vinakufa, yeye ni mama wa watoto yuko hapo na wala hatusaidii kuhakikisha kwamba, hawa wanaendelea kupata elimu na vyuo vile vinaendelea kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kipo Chuo cha St. Joseph Songea Mjini nacho pia hakifanyi kazi. Jana nilimtumia memo Mheshimiwa Profesa Ndalichako, nikasema naomba unieleze hivi vyuo vitafunguliwa lini? AJUCO ya Songea na Chuo cha St. Joseph cha Songea ni lini vitafunguliwa hivi vyuo? Maelezo aliyonipa kwa kweli, hayakuniridhisha na nasema Mheshimiwa Profesa Ndalichako leo hii wakati ana- wind up, naomba aje na majibu mazuri ya msingi ambayo yatani-stimulate niache kushika shilingi yake, vinginevyo nimpe taarifa kabisa kwamba, nakusudia kuzuia shilingi ya mshahara wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka niseme kwamba, hawa TCU wako kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, vyuo hivi vinaendelea kufanya vizuri, lakini kazi wanayoifanya sasa ni kuzuia, kukataza vyuo visiendelee; hatuwezi kusaidia vyuo hivi viweze kufanya kazi endapo kama utaratibu utaendelea kuwa huu. Ni vizuri sasa Serikali isimame na TCU wafanye kazi yao ya kuwaelekeza na kuwasaidia, kuwashauri, ili vyuo hivi viweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwetu Ruvuma kumekuwa doro, hakuna chuo chochote kile cha Serikali ambacho kitaweza kusaidia zaidi ya VETA, hakuna chuo kingine ambacho kitaweza kusaidia na uhitaji ni mkubwa sana. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Profesa Ndalichako awe makini na awe standby kabisa kwamba, nitazuia shilingi ya mshahara wako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani sasa kijengwe chuo kikuu angalau kimoja katika Nyanda za Juu Kusini ambacho kitasaidia hasa katika Mkoa wa Ruvuma. Kijengwe chuo kimoja ambacho kitasaidia ambacho kiwe na program kama tatu hivi. Chuo kikuu hicho kwa sababu sisi katika Mkoa wa Ruvuma tunalima mazao mchanganyiko sana, kwa hiyo, nadhani kwamba, kuwe na program tatu katika chuo hicho kitakachoanzishwa ambazo ni crop program. Crop program itasaidia kuendeleza shughuli za uzalishaji kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nyingine ni Chemical Engineering. Sisi tunalima kule korosho na kahawa, tulidhani sasa hii chemical engineering itasaidia hii program kuhakikisha kwamba, eneo lile linaendelea kustawi kupitia hizo program. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuna Ziwa Nyasa. Ziwa hili limetulia tu halina mwendelezo wowote. Kwa hiyo, nadhani kwamba, kukiwa na program ya fisheries itasaidia sana kuwainua vijana wetu na watafanya uwekezaji kwenye ziwa ambalo linaonekana. Mheshimiwa Profesa Ndalichako ni mtani wangu, lakini leo mimi sina utani naye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesisitiza sana kwamba, Wizara isaidie hivi vyuo. Nakumbuka Awamu ya Tatu ya Mheshimiwa Benjamin William Mkapa ilisaidia chuo ambacho ni University of Morogoro, University of Morogoro walisaidiwa wao walikuwa na shida ya majengo, lakini Mheshimiwa Rais aliweza kutoa maelekezo wakapewa majengo ya TANESCO na yale majengo yaliwasaidia. Sasa ni kwa nini Mheshimiwa Profesa Ndalichako hasaidii vyuo vya Songea vile vilivyofungwa ili viweze kufunguliwa? Ana ajenda gani wakati Kusini sisi kule hatuna chuo chochote? Tunamwomba tafadhali sana, yaani kule Mkoa wetu umepooza, hakuna vijana wanaoendelea katika shughuli za kusoma kupitia vyuo vikuu. Nakuomba sana, tafadhali sana, nilitaka kulia ila kwa sababu ni Mwezi Mtukufu, kwa hiyo nimeacha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni kwanini Mheshimiwa Ndalichako husaidii vyuo vya Songea vile vilivyofungwa ili viweze kufunguliwa? una agenda gani wakati kusini sisi kule hatuna chuo chochote tunakuomba tafadhali sana yaani kule Mkoa wetu umekuwa umepooza hakuna vijana wanaoendelea katika shughuli za kusoma kupitia vyuo vikuu. Ninakuomba sana tafadhali sana nilitaka kulia ila kwasababu Mwezi Mtukufu kwa hiyo nimeacha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Prof. Ndalichako naomba wasaidiwe hawa vyuo hivi vya taasisi za dini waweze kama kuna shinda ya majengo wapewe majengo lakini kama kuna shida ya fedha wapewe fedha, lakini pia kama kuna masuala ambayo yanahusiana na masuala la management nayo pia nimeambiwa kwamba ili chuo kiendelee lazima kuwe na ma-professors ina maana Mheshimiwa Prof. Ndalichako wewe ulikuwa Mwalimu wa vyuo vikuu huna ma-professors utupelekee kule vyuo vile vifunguliwe.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja nakusudia kushika shilingi ya Mheshimiwa Prof. Ndalichako. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, lakini pia namshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyenipa uzima hata niweze kusimama hapa katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kupongeza ushindi wa kishindo wa Majimbo mawili ya Kigoma; Jimbo la Buhigwe na Jimbo la Muhambwe. Kwa kifupi sana napenda niwataje makamanda ambao walikwenda kwa niaba ya Wabunge wengine wote kufanya kazi. Hawa walikwenda front line. Napenda kumtaja Major General Shangazi; Mheshimiwa Shangazi, pia Major Aeshi, Major Jacqueline Msongozi, Captain Bupe Mwakang’ata, Captain Mariam Ditopile na Afande Santiel, ambao walishiriki kikamilifu katika Jimbo la Buhigwe na kuhakikisha ushindi wa asilimia 83. Hongera nyingi sana kwao. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka sasa niende kwenye mchango wangu. Napenda kuzungumzia Daraja la Mkenda ambalo linakwenda Mitomoni…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline hivyo vyeo vya kijeshi sijajua kama mmetunukiwa kule au ndiyo unatunuku sasa hivi humu ndani! (Kicheko)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Hii ni katika shughuli mahususi, inaruhusiwa. Daraja la Mkenda kwenda Mitomoni Wilaya ya Nyasa kuna kivuko kinaitwa Limonga. Kivuko hiki kimekuwa na changamoto kubwa sana. Kivuko hiki kina upana wa karibia mita 100 kama sijakosea, lakini pia napenda tu kusema, Serikali hii badala ya kuweka tu kile kivuko cha kuwabeba wale watu na kuwavusha, basi lijengwe daraja moja kwa moja kwa sababu tayari imeshaleta maafa makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kivuko hicho tarehe 1 Julai, 2016 wananchi 10 walipoteza maisha akiwepo Zuhura, Awetu, Fadhili, Rajabu, Bahati, Khadija, Saidi, Selemani, Omari na Juni. Kana kwamba haikutosha, mwaka 2020 mamba alipindua mtumbwi. Sasa itoshe tu kuona kwamba Watanzania wenzetu wanapoteza maisha sana katika kivuko kile. Naiomba sana Wizara, ione umuhimu wa kwenda kuweka mikakati mizuri ambayo itasaidia na itaondoa adha hii ambayo imekuwa ikisababisha wananchi hawa wanapoteza maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie Bunge lako Tukufu hili kumwomba Waziri mwenye dhamana aongozane nami baada ya Bunge hili, pamoja na Mbunge wa Jimbo la Nyasa na Mbunge wa Jimbo la Peramiho, twende kwa pamoja kwenye kivuko kile kuhakikisha kwamba mikakati mizuri inawekwa kwa ajili ya kuokoa ndugu zetu hao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuzungumzia barabara ya kutoka Mtwara Pachani kuelekea Tunduru kupitia Ruchiri – Rusewa – Magazini – Narasi – Mbesa – mpaka Tunduru. Barabara hii ina urefu wa kilometa 300 ni barabara ya kimkakati ambayo itasaidia kurahisisha usafirishaji lakini kuchochea kasi ya uchumi katika Mkoa wa Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, napenda nizungumzie mpango mzuri wa Serikali wa kuhakikisha kwamba miji mikuu inapokuwepo basi barabara za pembezoni zinawekwa, barabara ambazo haziingiliani na mambo ya malori katikati ya miji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kuizungumzia barabara ya bypass ya kutoka Mretele kwenda Ruwiko ya Songea Mjini yenye urefu wa kilometa 11. Barabara hii imekuwa na msongamano mkubwa wa magari, bajaji na pikipiki. Imekuwa ni rabsha na ajali zimekuwa nyingi sana. Vilevile ni barabara ambayo ni ya muda mrefu sana; siku zote tumekuwa tukiambiwa upembuzi yakinifu, upembuzi yakinifu, jamani ni urefu wa kilometa 11. nikuombe Mheshimiwa Waziri funga macho, hebu nenda kajenge ile barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii niseme tu, huu ni mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba hakuna msongamano katikati ya miji. Tunaangalia katika Mji wa Iringa, hakuna msongamano, barabara ile kule chini inapita malori. Vile vile ukiangalia Mwanza na Dar es Salaam, hakuna msongamano wa malori.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie barabara ya bypass; nimekwenda Mbeya tukiwa ziara na Wabunge, tukafika Mbeya…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …Taarifa amekataa Naibu Spika. Mnanipotezea muda bwana! (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam.

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika... (Kicheko)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, anataka kukulisha maneno mdomoni huyu Mheshimiwa. Namshangaa anasema Mwanza hakuna msongamano; lini umetoka Mwanza wewe! Mwanza kuna msongamano wa kutisha kama Mbeya ilivyo na Dar es Salaam na Dodoma sasa hivi kuna msongamano. Majiji yote yana msongamano. Jiji huwezi kulinganisha na mkoa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tabasam!

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Naam!

NAIBU SPIKA: Ngoja kwanza. Kaa tu. Waheshimiwa Wabunge, nadhani nilieleza jana wakati tunafunga Bunge hapa. Misongamano inatofautiana. Kuna msongamano wa magari kushindwa kupita kabisa kwa sababu ya utelezi, kuna msongamano unaoweza kusababishwa na mvua kama Dar es Salaam ambako wanahitaji mitaro. Kwa hiyo, misongamano inatofautiana. Nadhani tuelewane hapo. Mheshimiwa Mbunge ukiwa na hoja, huwezi kumwuliza Mbunge, yaani unakuwa unampa taarifa, usimuulize swali kwa sababu siyo kazi yake yeye kujibu.

Wewe unampa taarifa kwamba, unaanza ukisema, naomba kumpa taarifa kwamba Mwanza kuna msongamano barabara moja, mbili, tatu; moja, mbili, tatu. Huwezi kumwuliza swali kwamba wewe umepita lini; na msongamano upo? Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, malizia mchango wako.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Tabasam hiyo siyo nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kama ifuatavyo. Mwezi wa Tatu, Wabunge…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Haya, muda wako umeisha Mheshimiwa, nakumbushwa hapa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …tulipata fursa ya kwenda Mbeya…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …na nilikuta kule kuna msongamano wa hatari sana. Kilometa 48.9 kutoka Uyole kwenda Songwe, sasa mimi niombe…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa Jacqueline.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Naunga mkono hoja. (Makofi/Kicheko)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana, na ninaomba Mwenyezi Mungu aniongoze katika mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, naanza na Chama cha Msingi cha UMANA katika Kata ya Lisimunji, Wilaya ya Namtumbo. Kwenye hiki chama kuna mgogoro mkubwa sana Mwenyekiti na viongozi wengine wa chama hiki wametumia fedha za chama hiki vibaya. Kwa hiyo, wananchi ambao ni wanachama wameamua kumkataa huyu Mwenyekiti, lakini kilichojitokeza sasa wakati wa zile vurugu za kumkataa yule Mwenyekiti Diwani alijitokeza akaenda kushirikiana na wale wananchi kwa ajili ya kutaka kujua hatma ya suala zima la chama hiki juu ya huyo mwenyekiti na viongozi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini viongozi kutoka wilayani kwa maana ya Serikali wakaenda wakamchukua yule Diwani wakamweka ndani, jambo ambalo si sawa, Diwani alikuwa anatetea haki za wananchi wake, lakini amewekwa ndani hii si sawa na niombe Serikali yangu, niiombe Serikali ishughulikie suala hili kupitia waziri mwenye dhamana aende akachunguze kule kulikuwa na tatizo gani na ikiwezekana huyu Diwani alipwe fidia kwa kufedheheshwa na kuwekwa ndani wakati akitetea maslahi ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ni kuhusu na suala la ushirika, ushirika kupitia AMCOS na UNION mimi nadhani kwamba hawa watu hawajajipanga vizuri, hawako sawa, kupitia AMCOS na UNION hawa watu hawana wanachokifanya cha kuwasaidia wanachama badala yake wameweka kama ni sehemu yao ya kujinufaisha wao wenyewe migogoro imekuwa mingi na wananchi hawasaidiwi kwa namna yoyote ile na ndiyo maana kumekuwa na kelele nyingi kuhusiana na suala la stakabadhi ghalani. Wananchi hawahitaji stakabadhi ghalani inayohusiana na mazao madogo madogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, stakabadhi ghalani imeletwa na Serikali kwa maana nzuri kabisa ili iweze kuleta tija na imefanya vizuri sana kwenye mazao makubwa kama korosho, pamba lakini kwenye ufuta, soya na mazao mengine madogo madogo ambayo yanakwenda kumsaidia mkulima haijafanya vizuri. Mkulima mdogo amelima ufuta maana ni zao ambalo linamsaidia auze aweze kujikimu kwa mambo madogo madogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali inavyoingilia kati na kusema kwamba mwananchi huyu apeleke zao hili kwenye stakabadhi ghalani maana yake ingekuwa ina tija kwa wananchi hawa wasingekuwa na kelele.

Mheshimiaw Spika, nitoe ushauri kwa Serikali hii, irudi ikajipange upya iondoe suala la stakabadhi ghalani kwenye mazao haya madogo madogo iache kwenye mazao makubwa kama korosho na mazao mengine lakini siyo ufuta. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Msongozi unapewa taarifa.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, napenda tu kumpa taarifa mzungumzaji, anayoyazungumza ni ya msingi zaidi na hii ndiyo sababu unaona Mkoa wa Dodoma leo hii hawalimi zao la ufuta. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Nakushukuru sana, Mheshimiwa Msongozi endelea.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, sasa mtani wangu wewe umechangia asubuhi halafu unanipotezea muda.

Mheshimiwa Spika, namba choroko, soya, ufuta hivi havina haja ya stakabadhi ghalani. Kwa mfano, wanawake wa Mkoa wa Ruvuma unapolima mahindi, korosho, tangawizi unaweka shamba dogo la mama kama kuna UPATU, VICOBA, kumpeleka mtoto zahanati na mambo mengine kadha wa kadha ndio ule ufuta unasaidia. Ukimwambia mwanamke achukue ule ufuta debe mbili apeleke huko akasubiri, mnamtakia nini huyu mwanamke wa Mkoa wa Ruvuma? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala hili haliwezekani asilani abadani. Mimi niwaombe Waziri na Naibu Waziri waje na majibu mazuri wakati wa wind-up waondoe suala hili la stakabadhi ghalani kwenye mazao madogo madogo. Mazao madogo madogo haya ni aibu jamani kwani ndiyo yanamsaidia mwananchi. Siku moja Mheshimiwa Flatei alisema ataruka sarakasi mimi kuhusiana na suala hili nauliza nipande juu ya meza? (Makofi)

SPIKA: Hapana.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Nipande juu ya meza kama Kanuni inaruhusu?

SPIKA: Mheshimiwa Msongozi usipande juu ya meza.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, kwa kweli kwa Mkoa wa Ruvuma hatukubali. Naomba suala hili liondolewe na Wizara ikajipange upya hata mwakani waje wakati wametoa elimu kwa wananchi lakini pia…

SPIKA: Mheshimiwa Msongozi usipande juu ya meza leo hapa kitaeleweka kuhusu stakabadhi ghalani. Waziri yuko hapa, leo hapa leo hapa, malizia Mheshimiwa Msongozi nilitaka tu usipande juu ya meza. (Makofi/Kicheko)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa sababu mimi nilisema leo labda ningepanda juu ya meza dunia ijue na Tanzania nzima waone kwamba hatuhitaji suala hili.

Mheshimiwa Spika, nikushawishi uniongezee dakika moja niendelee kuongelea suala hili. Wako vijana wetu wamemaliza vyuo, wametoka JKT wamefanya mafunzo lakini wamerudishwa nyumbani ajira hakuna. Hawa vijana wamejikita kulima mazao ambayo yanaweza kuwaletea pesa kwa haraka ikiwemo ufuta, soya na vitu vingine lakini wanakatishwa tamaa. Hili zao la ufuta sasa limekuwa kama vile mtu unalima bangi, ukishavuna debe mbili za ufuta basi unafuatwa unazingirwa. Hata mambo mengine ndani ya nyumba hayawezi kuendelea vizuri kwa sababu unafuatiliwa huko yaani muda wowote unagongewa kuulizwa zile debe mbili ziko wapi? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, vijana wetu hawa watakuwa majambazi sasa kwa sababu wanataka wawekeze kwenye ufuta lakini Serikali inawapiga danadana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Namshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa uzima ili niweze kusimama hapa leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza kabisa, naomba nichukue nafasi hii kuzungumzia Mkoa wa Ruvuma, Mkoa wa Ruvuma kwa maana ya kuugawa. Tunapozungumzia maendeleo, ukuaji wa uchumi katika nchi yetu ya Tanzania, imetosha tu kwamba tuzungumzie pia na mikoa ambayo ni mikubwa sana, mikoa ambayo kwa ukubwa wake inasababisha huduma za msingi zinashinda kufika kwa wakati na kuweza kutosheleza kwenye maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Ruvuma una population ya watu 1,376,891 kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012 na sisi kule watu wa Ruvuma tunazaana sana, mpaka sasa hivi maana yake wakija kufanya sensa tunaweza tukawa tumefikia watu 2,000,000. Kwa misingi hiyo, naomba sana Mkoa wetu wa Ruvuma uwe ni miongoni mwa mikoa inayoenda kugawiwa ili tuweze kupata mikoa miwili sasa uwe Mkoa wa Ruvuma na uwe Mkoa wa Selou na vigezo vipo na niseme tu kwamba hii ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne alipokuja Mkoani kwetu Ruvuma alizungumzia kuugawa huu mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkoa huu kwa kukuthibitishia tu naomba nitoe vigezo vya mikoa mingine ambayo ina population ya watu wachache sana, lakini imepata mikoa. Nataka nizungumzie Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Katavi una population ya watu 564,000 tu, tofauti na Mkoa wa Ruvuma ambao kwa sasa una watu 1,376,891. Mkoa wa Njombe una population ya watu 702,000 tu, Mkoa wa Lindi una population ya watu 964,000 kwa hiyo ni wazi kwamba Mkoa wa Ruvuma unakidhi vigezo vya kuongeza mkoa, kwa hiyo tunaomba tupate mkoa mwingine mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumshukuru sana Waziri wa Miundombinu ya barabara, lakini pia nimshukuru Waziri wa Fedha kwa namna ambavyo ametuheshimisha Wanaruvuma na niseme tu kwamba nampa big up sana Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama, Mbunge wa Jimbo la Peramiho ambaye barabara hii ya Likuyufusi – Mkenda inapita kwenye jimbo lake. Kwa pamoja yeye akifuatilia kwa ukaribu kabisa sambamba na mimi winga machachari ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimekuwa nikiizungumzia sana barabara hii yenye urefu wa kilometa 124 inayotoka Likuyufusi kwenda Mkenda ambayo inaunganisha Nchi ya Tanzania na Mozambique.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha akumbuke kwamba, sasa hivi hii ni bajeti yake ya kwanza akiwa Waziri wa Fedha na kikubwa kinachotakiwa ni kuendelea kujenga nchi yetu ya Tanzania iendelee kukua kiuchumi. Kwa hiyo barabara hii atakapoijenga itaendelea kufungua fursa nyingi za kiuchumi na kodi italipwa na nchi yetu itaendelea kukua, wananchi watapa ajira na wananchi wetu wa Mkoa wa Ruvuma wataendelea kunufaika na rasilimali za nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nataka nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mama yetu jemedari Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya, mwanamke shupavu, mwanamke mahiri, kwanza Mungu kamjalia, kwanza kabisa ukimwangalia sura yake nzuri, sura ya upole, mama mwenye upole, mama mwenye upendo. Kwa misingi hiyo mama huyu ana upendo mpaka ndani ya moyo wake, kwa bajeti hii ambayo imeletwa safari hii, ni bajeti ya kupigiwa mfano, bajeti nzuri ambayo imeenda kugusa moja kwa moja kwa wananchi wanyonge na kukwamua matatizo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niwaombe kupitia Bunge lako Tukufu, Watanzania wote waweze kumuunga mkono Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kulipa kodi. Watakapolipa kodi ndipo hapo tutapata maendeleo kupitia ujenzi wa barabara, umeme, maji, afya na elimu. Kwa misingi hiyo kulipa kodi ndiyo maendeleo ya nchi yetu. Niseme tu, kupitia malipo mazuri ya kodi, basi maana yake itakwenda kuboresha hata sisi Wabunge hapa, amesema mama yetu Mheshimiwa Samia kwamba anaanza na kuboresha mishahara ya watumishi, maslahi ya watumishi ikiwa pamoja na kuwaongezea vyeo vyao ili waweze kuendana na wakati huu wa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni imani yangu, atakapoboresha baada ya kodi kulipwa na sisi Wabunge hapa tutakwenda vizuri, mambo yetu yatakwenda vizuri. Itoshe tu kusema kwamba ikimpendeza Mungu panapo majaliwa kama jina litarudi wakinipa hawa nafasi maana yake nitasimamia katika kamisheni ya Bunge kuhakikisha kwamba maslahi ya Wabunge kupitia safari za kwenda nje ya nchi, kwa sababu Mbunge kama Mbunge ni lazima upate exposure, kwa maana ya kwenda kujifunza nje ya nchi katika nchi ambazo zimefanikiwa sana kwenye miundombinu, afya, elimu na mambo mengine mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo bila Mbunge kupata exposure maana yake tunakuwa tuna mawazo ya kwetu tu hapa ndani ya nchi bila kwenda nje ya nchi. Hii niwaambie tu ndugu zangu kama mkiniwezesha mambo hayo yakakaa vizuri maana yake nitasimama kindakindaki. Mjue kabisa kwamba uwezo ninao wa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nizungumzie suala la namna ambavyo Mama Samia ameboresha kwenye masuala ya Madiwani. Madiwani sasa hivi wanakwenda kulipa pesa zao kupitia Serikali Kuu. Kwa msingi huo kulipwa tu kupitia Serikali Kuu haitoshi, ilitosha tu hawa Madiwani waongezewe pesa. Madiwani hawa ndio ambao wanafanya kazi asubuhi, mchana, jioni wao ndio wanakutana na wananchi kule chini kwenye grass root kwa hiyo hawa Madiwani katika utendaji wao wa kazi bado mzunguko wa maeneo yao waliyonayo ni mkubwa mno kiasi ambacho sasa yule Diwani, wakati mwingine unakuta Diwani ana vijiji 12, 15, vijiji nane, vijiji tisa au vijiji 20. Kwa hiyo, naomba kupitia bajeti hii itoshe tu kwamba Waheshimiwa hawa Madiwani waweze kutengenezewa utaratibu wa kupata mkopo kwa ajili ya kupata usafiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huo usafiri utawasaidia kama vile ambavyo Makatibu Tarafa wameweza kusaidiwa usafiri, wakapata pikipiki, lakini pia Watendaji wa Kata wameweza kusaidiwa wanapata posho. Waheshimiwa Wabunge mengine hatuwezi kusema hapa, mkinipa kale ka mambo kale ndio nitasema vizuri huko na nataka niwaahidi kwamba nitakuwa shujaa wenu na sisi Wangoni tulishakuwa mashujaa, kwa hiyo huu ni mwendelezo tu, tulikuwa mashujaa, tumepigana vita na Wajerumani na hata nyie mkawa mna nafuu huko mliko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu kipenzi Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuchochea maendeleo katika nchi yetu ya Tanzania. Nimesimama hapa nikiwa kama Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria nami napaswa kuzungumza yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kazi ambazo zilifanywa kwa mwaka mzima, napenda zaidi kuzungumzia taasisi ambayo iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo inahusiana na masuala ya majanga ya usalama mahali pa kazi (OSHA) wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana. Pia Kamati ilibaini kwamba OSHA wana kila sababu ya kuongezewa watumishi kwa sababu watumishi walionao kwa sasa ni wachache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaangalia pia kwenye suala zima la taasisi ambazo zinashughulika na majanga mbalimbali ikiwemo Zimamoto. Kamati imebaini kuwa wenzetu hawa wa Zimamoto bado kimsingi hawajajipanga vizuri, kwa sababu hawana vitendea kazi, lakini pia maeneo mbalimbali ambayo majanga yanatokea wanashindwa kufika kwa wakati. Basi tumeona ni vizuri sana sasa tuishauri Serikali, iweze kuwezesha maeneo hayo ili mwisho wa siku haya majanga ambayo yanatokea na yamekuwa yakiwa yanaathiri sana uchumi wa wananchi na Taifa kwa ujumla; basi yaweze kusimamiwa vizuri na kuweza kuondokana na hiyo hali ambayo kimsingi huwa inaleta hasara kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kumekuwa na umeme mpaka vijijini kule, umeme wa REA umekwenda mpaka vijijini tunaishukuru sana Serikali kwa kufanya kazi nzuri namna hiyo, lakini sasa umeme huu umekwenda vijijini. Kuhusiana na masuala ya majanga mbalimbali wananchi je, wamepewa mafunzo maalum kuhusiana na masuala ya umeme? Faida zake na hasara zake incase kama hawatautumia vizuri umeme, nani ametoa maelekezo haya? Basi tumeona ni vizuri kuishauri Serikali kwamba, iweke kipaumbele kwenye kutoa elimu kwa wananchi kuhusiana na suala zima la umeme ambao umekwenda mpaka kule vijijini chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la taasisi nyingine ambayo iko ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu, PSSSF. PSSSF wamefanya kazi nzuri sana, tulikwenda pale Moshi kukagua Kiwanda cha Viatu ambacho PSSSF wana asilimia 86 na Magereza wana asilimia 14 kwa maana ya ubia. Kazi wanayoifanya ni nzuri sana lakini bado kuna changamoto kubwa sana kwenye vile viatu wanavyovitengeneza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viatu wanavyovitengeneza ngozi yake ni ngumu sana. Kwa mfano kama unamnunulia mtoto kiatu, basi unaweza kukuta katika viatu pea nne ulizonunua ukanunua na hicho ambacho kinatengenezwa na kiwanda kile, ukakuta mtoto anapenda kuvaa viatu vingine lakini kile anakiacha kwa sababu kile kiatu ni kizito. Pia bei zake is not affordable kwa wananchi wa kawaida. Kwa hiyo watakaonunua vile viatu ina maana ni wale watu ambao wana uwezo. Kwa hiyo sasa tumeshauri kwamba wenzetu hawa wajipange vizuri waweze kutengeneza viatu kuendana na hali ya sasa ili waweze kupata masoko ya watu wa kada tofauti tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapato ya ndani ya halmashari ni asilimia 10. Nimemsikia Mheshimiwa Mbunge mmoja amezungumza sikusudii kurudia lakini nadhani nikazie hapo hapo. Haya mapato ya ndani nia ilikuwa ni kuwasaidia makundi mbalimbali kwa ajili ya kuwawezesha kiuchumi, lakini kwa sasa hivi tunapata mashaka huenda fedha hizi zinatumika vibaya. Kwa mfano; tumesikia maeneo mbalimbali na juzi nimeona kwenye mtandao, mdogo wangu Jokate Mwegelo pale Temeke ameingiliwa na watu ambao kimsingi katika halmashauri ile unakuta Diwani mmoja ameweza kujiwezesha mpaka milioni 300 ya mapato ya ndani ya halmashauri. Maana yake amekwenda ameunda vikundi vikundi hatimaye amekwenda kujiwezesha yeye mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahusiano ya vikundi vile ambavyo vimepewa fedha yaani havina mahusiano ya ukaribu na halmashauri. Vikundi vingine vipo mbali, ni nje ya halmashauri husika. Kwa hiyo, niombe CAG aende akakague katika halmashauri zote ili aweze kujiridhisha kuhusiana na hii fedha ambayo ni asilimia 10 ya mapato ya ndani. Nia ni kumwezesha mwananchi ili aweze kujikwamua kiuchumi, lakini sasa inakuwa tofauti watu wanataka kujinufaisha wao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nizungumzie suala la Madiwani. Madiwani wamekuwa wakifanya kazi kubwa sana kwenye maeneo husika, sisi tupo hapa Bungeni muda wote wako kule na wananchi. Kwa misingi hiyo, wanatakiwa kwa hali na mali tuwatetee ndani ya Bunge hili ili waweze kuongezewa posho kwa sababu kazi wanazifanya lakini pia hawana usafiri wa kutoka eneo moja kwenda eneo lingine hasa wale Madiwani wa vijijini ambao kimsingi wanakuwa wanatoka kijiji fulani kwenda kijiji kingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya machache, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia bajeti ya mwaka 2020/2022 na 2020/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mimi nimchangiaji wa kwanza kabisa katika bajeti hii ya mwaka nilioutaja, ambayo inakadiliwa kuwa na thamani ya pesa za Kitanzania shilingi trilioni 41, naomba nichukuwe nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu na niseme rasmi kwamba sasa naliamsha dude. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakwenda moja kwa moja kwenye suala la kilimo. Suala la kilimo niseme kwamba sasa kimepata Waziri ambaye anaendana na kasi ya sasa ya kwenda kufungamanisha masuala ya kilimo na viwanda. Ni matumaini yangu kwamba akipewa bajeti itakayotosha, basi atakwenda kufanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge hili naomba niwajulishe Watanzania kwamba wasiwe na hofu kuhusiana na suala la kilimo, tayari linakwenda kupata tiba na ndugu zangu wa Mkoa wa Ruvuma sasa wanakwenda kupata tiba ya kile kilio cha mbolea kwa maana ya bei kubwa ya pembejeo zilizokuwa zimewekwa. Kwa mujibu wa taarifa ambayo juzi imetolewa na Waziri mwenye dhamana, anasema kwamba ana uhakika wa kuweka ruzuku kwenye mbolea na hatimaye mbolea hii itakuja ikiwa na bei ambayo inanunulika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kuomba taasisi mbalimbali za fedha kujitokeza kusaidia kwenye Mkoa wa Ruvuma walete pesa za mikopo ili wananchi wa Mkoa wa Ruvuma weweze kukopa waende kuwekeza kwenye kilimo. Naomba sana taasisi hizo zitukopeshe kwa style ya single digit ili kila mkulima aweze kukopa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mkoa wa Ruvuma ni bingwa kabisa na umeshika namba moja miongo minne mfululizo kwa uzalishaji wa mazao ya nafaka nchini, ni matumaini yangu kwamba Serikali itaona umuhimu pia wa kupeleka Benki ya Kilimo ili wananchi waweze kukopa kwa ukaribu. Hata mtoto akifanya vizuri, anapewa zawadi. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Serikali kwenda kuweka Benki ya Kilimo katika Mkoa wa Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na suala la EPZ kuchukua maeneo mbalimbali na kuwafanya wananchi kuendelea kuwa masikini kwenye maeneo husika bila kuwapa riba. Miongoni mwa maeneo hayo naomba nitaje Kata ya Mwengemshindo iliyoko katika Manispaa ya Songea. Hivi ninavyozungumza, kutokana na zoezi la anuani ya makazi, Mwengemshindo imetengwa na wananchi wana tafrani, hawaelewi mwisho wao, hawaelewi mwelekeo, kwenye eneo la makazi hawajahesabiwa nyumba zao. Kwa misingi hiyo, wanapata mashaka kwamba inawezekana wanaondolewa kwenye duru ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia EPZ wamechukua eneo la Mwengemshindo tangu mwaka 2008, mpaka sasa hivi ninavyozungumza ni takribani miaka 12 wananchi hawa hawajapewa fidia na wamedumaa kiuchumi. Serikali inachukua hatua gani ya haraka ya kuwawezesha hawa wananchi ili waweze kuondoka kwenye maeneo haya na waende kwenye maeneo mengine ambayo wataweza kwenda kufanya uwekezaji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pesa wanayoidai mpaka sasa hivi kutokana na eneo hilo ni shilingi bilioni 3.5. Naomba Serikali iniambie ni lini watawezesha wananchi hawa wa Kata ya Mwengemshindo ili waweze kuondoka maeneo hayo na kwenda kuwekeza maeneo wanayokwenda kutarajia kufanya shughuli zao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni muda mrefu sasa imekuwa ikitajwa barabara ya Njombe Songea ambayo haijafanyiwa ukarabati kwa muda mrefu na inahitaji ifanyiwe upanuzi. Naomba Serikali ije na majibu, ni lini itaanza kufanya ukarabati huo? Pia tunayo barabara ya kimkakati Likuyufusi - Mkenda inayokwenda kuunganisha Tanzania na Mozambique, ina urefu wa kilometa mia 124; ni barabara ya kimkakati. Tunaomba kujua ni lini Serikali itaanza kuijenga kwa kiwango cha lami? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la barabara ya Mtwara - Pachani kwenda Lusewa na Rasi mpaka Tunduru pia ni barabara ya mkakati, tunaomba sasa ianze kujengwa kwa kiwango cha lami. Lumecha - Londo kwenda kwa Mpepo, yaani inaunganisha Mkoa wa Ruvuma na Mkoa wa Morogoro, tunataka ianzwe kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya Msindo ni kituo cha muda mrefu sana. Wananchi sasa wamejitokeza kujenga jengo la upasuaji kwa kutumia pesa zao. Sasa Serikali ni lini itapeleka pesa ili iweze kuhakikisha kwamba lile jengo la upasuaji linakamilika na waweze kupata huduma?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la utawala bora. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana kipenzi chetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, mwanamke shupavu ambaye amejipambanua ndani ya nchi na nje ya nchi, anafanya vizuri sana; na kwamba anafanya kazi zake kwa kuzingatia misingi ya utawala bora na anakwenda vizuri mno. Tuna imani naye, hatuna mashaka naye, mama yetu atatuvusha vizuri sana. Tunamwombea kwa Mwenyezi Mungu amjalie kila la kheri na kila atakapoona kwamba kuna jambo ambalo linakuwa ni kikwazo katika kutimiza majukumu yake kupitia masuala ya sheria, shime atuletee sheria hapa Bungeni tuzirekebishe na mambo yake yasikwame. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema kuhusiana na suala la utawala bora. Mheshimiwa Mama Samia anakwenda mwendo kasi, lakini wako baadhi ya watendaji wanamkwamisha. Tunaomba watendaji wote wa nchi hii wafanye kazi kwa uadilifu na uaminifu ili mama yetu asikwame mahali popote pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka nizungumzie suala la LATRA. Nchi yetu ni nchi ambayo hiko katika hali ya usalama kabisa, lakini pia tunatakiwa tuweke mazingira mazuri ya wananchi kufanya shughuli zao ikiwemo wajasiliamali waweze kusafiri muda wote, wasafiri mchana, wasafiri usiku. LATRA wana mpango gani wa kuhakikisha jambo hili linatekelezeka ili wananchi waweze kusafiri?

Mheshimiwa Naibu Spika, wako baadhi ya Watendaji Wakuu ambao ni tatizo kuhusiana na suala hili hili la utawala bora. Unampigia simu Mtendaji Mkuu unajitambulisha kwamba mimi ni fulani bin fulani. Sasa kama mimi kiongozi ninaweza nikajitambulisha na bado asirudi kwangu, asijibu message, hao ni watu ambao ni majipu yanatakiwa yatumbuliwe haraka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii pasipo shaka yoyote na nina ushahidi wa kutosha, ninaomba kama kanuni inaruhusu nimtaje Mtendaji wa LATRA ni jipu. Mtendaji Mkuu wa LATRA ni jipu. Hapokea simu, hajibu message, watu wanapata ajali maeneo mbalimbali, wafanyabiashara wana shida mbalimbali ya kujua ABCD, maeelekezo mengi anapata lakini hawezi kuyatekeleza. Sasa huyu ni mtu wa aina gani? Ingekuwa ni amri yangu ningesema apishe uchunguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niende kwenye suala la mpango mzima unahusiana na masuala ya vijana. Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia bajeti yake, ameeleza namna ambavyo vijana wamewezeshwa kwenye maeneo mbalimbali na tumeona vijana, mimi ni Mjumbe wa Kamati hiyo, tumeona vijana wamewezeshwa vitalu nyumba kwenye maeneo yao, lakini je mrejesho ukoje? Tathmini ikoje? Hawa vijana kupitia hivyo vitalu nyumba vimewasaidia kwa kiasi gani? Wame-achieve nini? Kwa hiyo, tunataka kujua.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata taarifa maeneo mengine unakuta Madiwani wanaingilia kati, wanapoka vile vitalunyumba vya vijana. Kwa hiyo, naomba sana Serikali yangu iende kule, Wakurugenzi wa maeneo husika waende wakakague na tupate majibu, vimesaidia kwa kiasi gani na vijana wamenufaika kiasi gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la mwisho, naomba sana wanawake wa Mkoa wa Ruvuma wana uhitaji sana wa kuwekeza katika kilimo. Naomba sana uwepo mpango mzuri; wakati mwingine unaweza kuwakopesha vikundi mbalimbali wakafanya biashara, lakini hawana utaalamu wa mambo ya biashara, lakini tukiangalia maeneo mbalimbali kulingana na jiografia zao na mila zilizopo, unaweza kuwasaidia vikundi hivyo ukawapa mbegu, ukawawezesha katika masuala ya kilimo na wakafanya vizuri zaidi na wakawa na tija zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno haya, naomba kuwasilisha. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi. Naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kupata fursa hii ili nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwenye Bajeti hii ya mwaka 2023/2024. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaenda moja kwa moja kwenye hoja mahususi kabisa inayohusu Kiwanda cha SONAMCO, kiwanda ambacho ni cha usindikaji wa tumbaku. Kiwanda hiki kimesimama kwa muda mrefu sana, toka mwaka 2010 mpaka hivi sasa kiwanda hiki hakijawahi kufanya kazi na, kiwanda hiki kiko Mkoani Ruvuma katika Wilaya ya Songea katika Manispaa ya Songea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Desemba mwaka 2022 Mheshimiwa Waziri Mkuu aliita wadau mbalimbali, wadau wa tumbaku na walikuja pale Songea na ukafanyika mkutano mkubwa sana ambao kimsingi mkutano huu umezaa matunda mazuri sana. Nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa jitihada hizi ambazo anazifanya hasa katika kuangalia ustawi wa Mkoa wa Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkutano huo pamoja na mambo mengine, kulijadiliwa namna gani ya kuweza kufufua Kiwanda cha SONAMCO Kiwanda cha Usindikaji wa tumbaku ambacho kiwanda hiki endapo kitaanza kufanya kazi, maana yake kina uwezo wa kuajiri wananchi 3,000 ambao watakuwa wananufaika na kiwanda hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni ya Vodsen Tobacco Limited ndiyo ambayo ilionesha nia ya kuwekeza na kuweza kufufua kile Kiwanda cha SONAMCO cha Songea Mjini. Kwa hiyo, sasa kupitia Bunge lako hili Tukufu, naomba nichukue nafasi hii sasa kumwomba Waziri wa Viwanda na Biashara ili aweze kuwapa uwezeshaji kampuni hii ili waweze kuja kuwekeza katika kiwanda hiki na kiwanda hiki kiweze kufanya kazi mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, naomba nichukue nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Hussein Bashe ambaye amekuwa akifanya kazi nzuri ya kuhakikisha kwamba anainua Sekta ya Kilimo, pia Mkurugenzi wa Bodi ya Tumbaku Tanzania, kaka yangu Stanley Mnozya ambaye amekuwa akifanya kazi nzuri, hata kufikia hatua hii ya kiwanda hiki sasa kuweza kuanza uwekezaji wa kuinua kiwanda hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende kwenye suala la Twiga na Tanga Cement. Nimesikiliza toka asubuhi, Wabunge wengi humu ndani wamechangia, nami nikawa najiuliza tu, hata kama ninatoka Ruvuma ambapo tunahudumiwa kwa ukaribu sana na cement ambayo inatoka katika kiwanda cha Dangote, lakini nimesikia kilio cha Wanatanga wenzetu. Kwa kuwa wana Tanga ambao wamekuwa wakililia suala hili la cement kwa maana ya Kiwanda cha Tanga Cement kuendelea kuwepo hai, nikajaribu kujiuliza, ni nini ambacho kinasababisha? Nimegundua yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Twiga Cement wanataka kununua Kiwanda cha Tanga Cement, lakini katika ununuzi wao maana yake, endapo watanunua hizo shares, tayari Twiga Cement watakuwa wanamiliki share zaidi ya 68% ambayo kimsingi sheria inakataza. Suala hili linakinzana na sheria ambayo tumeitunga wenyewe katika Bunge lako hili Tukufu. Sasa najiuliza, ni kwa nini Serikali inadhamiria kwa makusudi kuvunja sheria hii? Kwa nini Serikali isirudi nyuma na kukaa chini kuanza mchakato huu upya ili kupitia na kuhakikisha kwamba utaratibu huu unafanyika chini ya sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nichukue nafasi hii kumwambia Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, zisikilize kelele hizi za wengi. Sauti ya wengi ni sauti ya Mungu. Urudi tena upya kwa ajili ya mchakato huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nishauri Bunge lako Tukufu hili kwamba mchakato huu uanze upya hapa tayari mchakato haujakaa sawa sawa. Kwa sababu kama mchakato umeenda vizuri hakukuwa na sababu ya kelele nyingi ambazo zimekuwa zikipigwa humu ndani, mchakato urudi upya lakini pia sheria izingatiwe hakuna sababu ya kukanyaga sheria ambayo tuliitunga sisi wenyewe kuna sababu gani? Sioni kwanini sheria ivunjwe kwa makusudi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, jambo jingine naomba niseme kwa kuwa jambo hili linasimamiwa chini ya Baraza la ushindani naomba baraza la ushindani liheshimiwe katika maamuzi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine la mwisho kwenye eneo hili marekebisho ya sheria kama sheria hii inakinzana na maamuzi ambayo yanataka kufanyika dhidi ya uwekezaji huu. Basi sheria hii irudi hapa tuirekebishe sheria kwanza badala ya kuikanyaga sheria na baada ya kurekebisha sheria ndiyo mchakato huu tuendelee nao. Aidha, kufanyike mapitio upya ambayo yatapelekea sasa mchakato huu kwenda vizuri na niseme tu kama kutakua kuna jambo lisiloeleweka zaidi basi nimuombe Mheshimiwa Spika aunde Tume kwa ajili kuchunguza jambo hili hatimaye jambo hili liweze kuleta majibu sahihi ambayo wananchi wa Tanzania wanamatumaini na Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie suala la Matrekta ya URSUS, haya matrekta yamekuwa yakilalamikiwa sana na matrekta haya yameletwa kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara. Hata hivyo mpaka sasa hivi wananchi ambao walinunua haya matrekta wamekuwa wakilalamika, wamekuwa wakisumbuliwa na makampuni mbali mbali ambayo yanahusiana na madalali, Takukuru. Ingawaje Takukuru sasa hivi awafanyi hiyo kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niseme kwamba tunaomba sana mchakato huu wakufatilia jambo hili kama vile ambavyo Mheshimiwa Spika aliamua kulichukua na kulifanyia kazi kwa ukaribu nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Spika wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Ackson Mwansansu kwa uamuzi wake aliyouchukua na kwamba sasa mchakato huo uende kwa haraka ili wananchi wawe na amani. Tumekuwa tukipigiwa simu, wengine wanakimbia majumba yao hawana amani kwenye maisha yao lakini bado wamefilisika na yale matrekta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matrekta ni mabovu, unachukua tu trekta kitendo cha kuwa jipya kabisa unaliingiza shambani, unaambiwa na fundi limekatika mgongo mara limekatika sijui kifudifudi. Kwa hiyo, haya matrekta hayana nia njema kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, niombe Wizara pamoja na eneo ambalo Mheshimiwa Spika ameona wafanyie kazi jambo hili waharakishe huu mchakato hili wananchi waendelee kuwa na amani kwa sababu kinacho endelea huko mitaani inawezekana kabisa tukapata majibu ambayo siyo mazuri kwa wananchi yanayoendelea huko mtaani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, EPZ naomba leo nizungumze na Waziri mwenye dhamana hii. Kwenye eneo hili la Viwanda na Uwekezaji EPZ walichukua maeneo ambayo yako kwenye Kata ya Mwenge Mshindo Wilaya ya Songea Mjini Manispaa ya Songea. Maeneo haya kimsingi yana miaka karibu kumi na tano wananchi hawajalipwa fidia ninaomba Waziri atakapokuja aeleze Aidha, kama hawezi kulipa pesa zote shilingi bilioni tatu na milioni mia nane azikate pale katikati alipe kwa awamu mbili tofauti wananchi wale wanateseka wamekuwa wadumavu hawana maendeleo yeyote, hawawezi kuendeleza chochote kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana jambo hili uweze kulishughulikia na utakapo kuja hapa na niseme Mheshimiwa Waziri endapo kama jambo hili utotoa majibu yanayoeleweka ninakusudia kuondoka na shilingi yako. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia Bajeti ya Wizara ya Kilimo ya mwaka huu 2023/2024. Naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya, lakini pia kwa maboresho makubwa sana kwenye Wizara ya Kilimo. Halikadhalika niwapongeze sana Waziri na Naibu Waziri na delegation yao yote kwa namna ambavyo wanafanya kazi kubwa ya kuinua Sekta hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, udhibiti wa ubora wa mbegu; naomba nizungumzie suala la udhibiti wa mbegu katika nchi yetu. Naomba kwenye eneo hili itumike teknolojia ya juu zaidi kwenye uandaaji wa mbegu. Kwa sababu tunaona mbegu ambazo tunanua nje ya nchi yetu ya Tanzania zina ubora zaidi na mimi nitakuwa shahidi kwenye mbegu aina ya Pannar 53, mbegu ya mahindi ambayo niliinunua mwezi Desemba pale Nchini Mozambique.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii mbegu inafanya vizuri sana, lakini nilipoulizia ndani ya nchi nikaambiwa kwamba hii mbegu haijathibitishwa, haitakiwi iletwe huku nchini. Sasa vitu vizuri kama hivi sisi tunachelewa kuchukua maamuzi. Mbegu hii Mheshimiwa Waziri kama atapenda twende shambani kwangu kabla sijavuna ili ashuhudie namna mbegu hii ya Pannar 53 ilivyobeba mahindi mawili mawili na yote yana afya. Kwa hiyo, naamini kabisa endapo kama mbegu hii pia itaingizwa nchini itaongeza tija kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie sasa mnyororo wa thamani ya mazao. Mheshimiwa Waziri anafanya kazi nzuri sana na tunaona sasa Wizara ya Kilimo inashika kasi. Kasi ya hali ya juu yaani unaweza kufananisha na kasi ya standard gauge railway, hongera sana lakini nataka nizungumzie kwenye masuala ya mazao haya. Mheshimiwa Waziri pamoja na kazi nzuri sana anayoifanya ya uzalishaji, lakini sasa hebu twende mbele zaidi wafikirie namna ya kuongeza mnyororo wa thamani kwenye mazao hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kwa mfano kwenye Mkoa wetu wa Ruvuma, ni kwamba mkoa huu ndio ambao unaongoza na umeshika nafasi ya kwanza mara nne mfululizo katika uzalishaji wa mazao ya nafaka Nchini Tanzania. Pasipo shaka yoyote hata mwaka huu tutaongoza halikadhalika. Sasa hebu twende sasa tutoke hapa tulipo kwenye kuuza mazao kama mazao Waziri atuongozee tuweze kupata sasa viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri atuambie kwenye mahindi sasa atapeleka viwanda vingapi vya kuchakata sembe, kwenye soya atapeleka viwanda vingapi vya kukamua mafuta na kwenye alizeti atapeleka viwanda vingapi vya kukamua alizeti ili tuweze kuuza bidhaa ambayo imekamilika. Tukifanya hivyo, itasaidia sana kumwinua mkulima, itaongeza ajira, lakini pia itasaidia kuingiza pesa za kigeni baada ya kuwa tumeuza mazao hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tumbako; Mheshimiwa Waziri naomba niseme kwamba wananchi wa Mkoa wa Ruvuma wamefurahia sana sana namna ambavyo Waziri amekuwa ukisimamia vizuri kwenye eneo hili la zao la tumbako na kwamba sasa suala la tumbako halijawa ni mzigo kwenye Mkoa wetu wa Ruvuma. Suala la tumbako limeleta ustawi katika wananchi wetu wa Mkoa wa Ruvuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapozungumza sasa hivi ni kwamba, miaka miwili iliyopita Mkoani Ruvuma tulikuwa tunazalisha tumbako tani laki tatu…

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi ninapozungumza tunazalisha tumbako tani milioni tisa…

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba jamani taarifa mzishikilie, nina mambo ya msingi sana ya kuchangia hapa leo, tafadhali sana.

TAARIFA

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, namwambia dada yangu sio tumbako ni tumbaku. (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Taarifa hiyo Mheshimiwa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, hizi taarifa nyingine saa nyingine zinakuwa zinapunguza hadhi fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nirekebishe hapo kwenye tani 500 za tumbaku. Ilikuwa tani 500 ndio ambazo zinazalishwa miaka miwili iliyopita, lakini sasa hivi zinazalishwa tani milioni tisa na kwamba wawekezaji na wanunuzi wamepatikana. Nichuke nafasi hii kuwapongeza sana wale wanunuzi wanaonunua tumbaku katika Mkoa wetu wa Ruvuma. Hali kadhalika nampongeza Mheshimiwa Waziri, nampongeza Mheshimiwa Rais, nampongeza pia Mkurugenzi wa Tumbaku Tanzania kwa kutusaidia kutafuta wadau mbalimbali ambao kimsingi wameleta ushindani na hatimaye sasa tumbaku katika Mkoa wa Ruvuma inaleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwa tumekuwa na uzalishaji huo sasa umefika mahali Mheshimiwa Waziri atambue wazi tuna uhitaji mkubwa wa Kiwanda cha Sontop pale Songea na kwamba sasa tumbaku hii inayozalishwa katika Mkoa wa Ruvuma iende ikachakatwe pale pale. Juzi nimeongea kwenye Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara, lakini nimeona uko umuhimu wa kurudia tena ili Waziri mwenye dhamana asikie. Kama kuna jambo linasubiriwa kwa hamu sana katika Mkoa wa Ruvuma, basi ni Kiwanda cha Uchakataji wa Tumbaku cha Sontop. Kiwanda hiki kinaweza kuajiri wananchi 3,000 ambao kimsingi utasaidia kukuza pato katika mkoa wetu wa Ruvuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu; ninapozungumzia suala la miundombinu nataka nizungumzie suala la Bonde la Kimbande ambalo liko pale Nyasa katika eneo la Mbaba Bay. Bonde hilo ni la muda mrefu linafanyiwa kazi lakini miundombinu yake imechakaa sana. Kwa hiyo, tunaomba kupitia Wizara hii waje waturekebishie ili vijana waweze kuendelea kuwekeza kwenye bonde lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Bashe, tunampongeza sana kwa sababu amefanya kazi nzuri na anastahili kupongezwa. Kuna mambo ambayo yanafanyika katika uboreshaji wa miundombinu, ujenzi wa maghala, vihenge, pikipiki kwa Maafisa Ugani, vinasaba kwa Maafisa Ugani lakini pia nataka nizungumzie kwenye eneo hilo, kwamba wakati Waziri akiwasilisha nilimsikia amezungumzia suala la kuhakikisha kwamba anawatafutia magari Maafisa Kilimo wa Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni jema sana. Naomba uboreshaji huo uende sambamba na kutafuta zana za kilimo ambazo zitamsaidia mkulima kwa sababu mpaka sasa hivi tunavyozungumza katika Mkoa wangu wa Ruvuma pamoja na kushika nafasi ya kwanza, lakini bado wamekua wakitumia jembe la mkono. Kwa hiyo ni vizuri sasa Mheshimiwa Waziri aje na mkakati mzuri badala ya kuuziwa matrekta mabovu ya URSUS…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante. Kengele ya pili hiyo.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Eeh! My Jesus Christ. Nimalizie?

NAIBU SPIKA: Ahsante, kengele ya pili.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ninapenda kumalizia nyongeza ya mchango wangu kwa Wizara ya Kilimo kwa kuwa wakati ninachangia ndani ya Bunge kwa kuwa muda ulikuwa hautoshi sikumaliza kuwasilisha mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, ninashauri suala la BBT liwekezwe zaidi kwenye mikoa na ukanda wenye uhakika wa mvua ili kuepuka gharama za ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji kwenye maeneo ambayo hayana nvua kabisa. Ninaomba pia kwa kuwa Mkoa wa Ruvuma umekuwa na uhakika wa mvua za kutosha, BBT ipelekwe huko mapema sana nina imani itafanya vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, kuhusu miundombinu; Mheshimiwa Waziri Hussein Bashe ameweka mpango mzuri sana wa kuweka miundombinu mizuri kwenye suala la utekelezaji na nitataja baadhi tu ya vifaa ambavyo ni pikipiki, vinasaba, nyumba, magari ambayo ametaja kuwa magari hayo yatawahusu Maafisa Kilimo wa Wilaya.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu sijasikia maboresho ya miundombinu kama magari yakitajwa kwa Wakurugenzi wa Taasisi za Wizara ya Kilimo kwa maana ya maslahi yao. Hawa wakurugenzi wanafanya kazi nzuri sana na ndiyo maana Wizara hii imeonesha matokeo chanya katika utendaji wake.

Mheshimiwa Spika, iko haja na ni jambo muhimu sana kwa wakurugenzi hawa kuboreshewa maslahi yao ikiwa ni pamoja na kuwapa magari mazuri yenye uhakika na yatakayokidhi mazingira halisi ya utendaji wao maana hawa viumbe wanazunguka nchi nzima kuhakikisha ustawi wa Wizara, wananchi na uchumi wa nchi unakuwa kama ilivyo sasa. Aidha kwa kuwa hawa wakurugenzi wamekuwa wakifanya kazi na makampuni makubwa yaani matajiri wakubwa ambao wana fedha nyingi ambazo zinaweza kuwaweka katika hali ya majaribu makubwa sana, ni imani yangu kuwa endapo maslahi yao yataboreshwa itasaidia sana kuwaongezea ari ya utendaji wa majukumu yao.

Mheshimiwa Spika, nipende kuliambia Bunge lako tukufu kuwa katika hali ya kawaida nimeona gari la mmoja wa wakurugenzi akiwa ziarani Mkoani Ruvuma katika kufuatilia majukumu yake kwa zao la tumbaku kwa kweli lile gari linaonekana kuchakaa kabisa, nikajiuliza ndio gari analotumia Mkurugenzi kuzungukia nchi nzima? Kimsingi magari kama hayo ni hatari sana kwa usalama wa watendaji hao, hata hivyo viumbe hawa ni rasilimali ya Taifa na inapotokea wanapata ajali na kupoteza maisha mara nyingi tunakuwa tunasema maneno rahisi kabisa kwamba "Taifa limepoteza kiongozi muhimu sana na kwamba pengo lake halitazibika" so what?

Mheshimiwa Spika, hii ni hatari sana na ni hasara kubwa kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mbolea ya ruzuku mfumo uboreshwe kwani inaonesha kuwa mfumo wa mbolea ya ruzuku ina tundu. Aidha, mbolea sasa ipelekwe mpaka vijijini ili kumpunguzia mkulima gharama na adha mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wafadhila endapo nitamaliza mchango wangu bila kuwataja watu wafuatao na ninaomba majina yao yaingie kwenye Hansard.

Mheshimiwa Spika, Watendaji Wakuu hawa wa taasisi ndani ya Wizara ya Kilimo wanastahili pongezi, wanafanya kazi nzuri sana hakika wanazitendea haki nafasi zao walizopewa nao ni hawa wafuatao; NFRA ni CPA Milton Lupa; Kahawa ni Ndugu Primus Kimaro; Korosho ni Ndugu Francis Alfred; Tumbaku ni Ndugu Stanley Mnozya; TFRA ni Dkt. Stephan Ngailo na CPB ni Ndugu John Maige.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa nafasi hii ninaunga mkono hoja na ninaomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JACQULINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia bajeti hii ya miundombinu ya mwaka 2023/2024. Naomba nianze kwa kumshukuru sana Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaifanya na pia kwa miundombinu mizuri sana ya barabara ambazo zimeweza kujengwa katika Mkoa wetu wa Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea nataka tu nikueleze kwamba sisi wana Ruvuma tumebaini kwamba Mheshimiwa Mbalawa kumbe si Mbalawa ni Mbawala wa kwetu Ruvuma. Kwa hiyo amefanya ujanja ujanja tu wa kubadilisha jina ajiite Mbalawa ili akwepe majukumu ya kupeleka miundombinu kule Ruvuma. Kwa hiyo wana Mbawala wenzako wamenituma niseme haya yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya bypass ya kilometa 16 ya Songea Mjini ambayo ni barabara yenye urefu wa kilometa 16, inatoka Mletele kwenda Msamala mpaka Namanditi. Miaka mitano iliopita nikiwa hapa katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimeshaizungumza zaidi ya mara nne, na barabara hii ilikuwa wakati naizungumzia ilikuwa na urefu wa kilometa 11, sasa hivi zimezaliwa kilometa nyingine, sasa ina urefu wa kilometa 16.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa Mheshimiwa Waziri alete pesa ili tujenge ile barabara. Kuna msongamano mkubwa sana katika Manispaa ya Songea, malori ni mengi mno yanayobeba makaa ya mawe. Jamani makaa ya mawe yanayopita katikati ya mji kwa kubebwa na malori ni zaidi ya malori 1,000 kwa siku. Ndugu zangu naomba mtusaidie. Kumekuwa na ajali nyingi sana kumekuwa na mitobozano mingi sana kati kati ya mji. Kwa hiyo tunaomba, ili kuwanusuru wananchi wa Manispaa ya Songea tujengee ile barabara ya bypass ya kilometa 16 ili sasa mji wetu uweze kuendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Namtumbo – Tunduru, kwa maana ya Mtwara Pachani kwenda mpaka kule Lingusenguse na hatimaye kufika Mbesa, Mbesa - Tunduru, barabara hii ina urefu wa kilometa 303. Feasibility study tayari imekwisha fanyika, tatizo ni nini barabara hii haitangazwi ili kuleta fedha na iweze kuanza kujengwa? Mheshimiwa Mbawala mwenzetu, tunakuomba sana utusaidie ili barabra hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa barabara ya Likuyufusi - Mkenda yenye urefu wa kilometa 24, niishukuru sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na jitihada zinazofanywa na dada yangu Jenista Mhagama na mimi pia nasema tena, maana ninasema kila siku humu ndani. Kilometa 60 za Barabara hii tayari Serikali imeonesha commitment ya kuanza kuijenga. Sasa kuonesaha commitment ni jambo zuri lakini tunataka mafungu yaende ili sasa ianze kujengwa mwaka huu wa fedha. Barabara hii itajengwa kilometa 60 kutoka Likuyufusi mapaka pale Mkayukayu. Sasa tunataka Serikali iweke pia commitment kutoka Mkayukayu mpaka pale Mkenda, kilometa 64, ili ianze kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoka hapo Mkayukayu hakuna commitment yoyote ya Serikali. Barabara hii ina urefu huo, kwa hiyo mkijenga kipande nusu halafu baadaye inasubiri tena miaka mitano hainogi kwa hiyo malizieni kilometa 124 zote ziwe na commitment ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya urefu wa kilometa 35 Kitai – Ruanda mkandarasi yuko kazini lakini barabara hii ni barabara ambayo itagharimu pesa za Kitanzania bilioni 60. Lakini mapaka sasa hivi mkandarasi amepata advance ya asilimia 10 tu ambayo ni sawa na bilioni 5.9. Mkandarasi anashindwa kuendelea na kazi, karibu anasimama kabisa na wakati huo huo tunaelekea kwenye masika, tunaomba sasa…

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jacqueline, kuna taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Taarifa iwe ya maana na mnanijua. Taarifa iwe ya maana.

MWENYEKITI: Karibu Mheshimiwa Benaya.

TAARIFA

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kumpa taarifa mchangiaji kuhusu barabara hii ya Kitai Kwenda hadi Ruanda na inaelekea hadi Lituhi. Mkandarasi amesimama tangu mwezi wa pili kwa sababu ya kukosa malipo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jacqueline taarifa unaipokea?

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Makofi mengi sana kwa Benaya. Nimeupokea mchango huo. Ahsante sana, nataka taarifa zenye afya kama hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyofafanua na inapita kwenye jimbo lake, ni sahihi kabisa kilometa 35 ambazo sasa ndio magari yale yanayobeba makaa ya mawe yanapita kwenye barabara hiyo. Kwa hiyo tunaomba pesa iharakishwe kupelekwa pale ili barabara hii iweze kujengwa. Kutokufanya hivyo maana yake ni kudumaza hali ya uchumi katika Mkoa wa Ruvuma na katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hadhalika Ruanda – Lituhi ameshanisaidia hapo Benaya kilometa 50 mkamalizie pale. Imetangazwa lakini pesa hazijapelekwa. Kutangazwa ni jambo moja, kupeleka pesa ni jambo jingine. Sasa Mheshimiwa Mbalawa mwenzetu tunaomba upeleke pesa kule ili barabara hizi zianze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nizungumzie suala la reli, kwa maana SGR. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri sana anayoifanya. Majuzi amesema kwamba miradi yote iliyoachwa na Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli anahakikisha anaimaliza kwa asilimia 100. Ninampongeza kwa sababu kazi ya SGR inaendelea. Hali kadhalika nimpongeze sana CEO wa SGR ambaye ni kaka yangu Kadogosa ambaye anafanya kazi nzuri sana. Kaka yangu Kadogosa wewe fanya kazi kelele za chura hazimzuii tembo kunywa maji, hizo ndizo changamoto za kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama wajumbe wa kamati ya PAC tumekwenda tumekagua namna mradi unavyoenedelea. Mradi ni mzuri mabehewa ni mazuri, hayo mengine yote ni majungu, endelea kufanya kazi na Mungu akutie nguvu, endelea kupambana, sisi tuko nyuma ayako tutaendelea kukutia moyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie sasa reli ya Mtwara – Mbamba Bay. Mimi naomba sana, ninaamini kabisa Mheshimiwa Mbawala hajaona yale malori ambayo yanabeba makaa ya mawe kule. Angeyaona huyu Mheshimiwa Mbawala mwenzetu kwa kweli angeweza kuchukua jukumu la kuharakisha ujenzi wa reli kutoka Mtwara Kwenda mpaka Mbamba Bay kwa sababu hali ya barabara sasa hivi ni mbaya. Malori yale yanachimba barabara haiwezekani. Ukiangalia barabara ambayo imetengenezwa hivi karibuni inayotoka Songea kwenda mpaka Tunduru pale katikati pale Namingwea mashimo yanafikia hapa kiunioni. Ndugu zangu hali ni mbaya sana. Kwa hiyo tunaomba sasa reli hiyo ikijengwa kwa haraka itarahisisha sana ubebaji wa mizigo, badala ya kubeba kidogokidogo basi itapakia mabehewa mengi na yatasafirishwa kwenda katika Bandari ya Mtwara na kupeleka maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie makaa ya mawe yaliyoko katika Mkoa wa Ruvuma ni makaa super ni grade number one, na ndiyo maana yamekuwa na wateja wengi sana. Daraja ya Mitomoni mwaka jana namalizia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia dakika mbili.

MWENYEKITI: Malizia sekunde 30.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, daraja Mitomoni mwaka jana nilipiga magoti hapa Mheshimiwa Mbawala wewe utapata laana na wana Ruvuma. Daraja lile halijajengwa watu wanaendelea kufa pale.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jacqueline…

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jacqueline, Mheshimiwa Mbunge…

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Litengwe kilometa 22 tunaomba kujengwa Kigonsela kilometa 35. Baada ya maneno hayo machache…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Jacqueline anaitwa Profesa Mbarawa naomba uendelee kumuita Mbarawa na siyo Mbawala.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, yeye anaelewa na ndiyo maana anacheka.

MWENYEKITI: Nashukuru sana, muda wako umeisha nashukuru sana Mheshimiwa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Ahsante sana, naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa fursa hii, lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uwezo wa kusimama hapa leo.

Mheshimiwa Spika, nami naomba niwe miongoni mwa wachangiaji kwenye hoja hii ya kuridhia kuanzisha mahusiano ya nchi hizi mbili; Tanzania na Dubai kwa ajili ya suala la uwekezaji kwenye bandari yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwanza mimi naona kwamba jambo hili limechelewa, yaani kwamba mchakato huu umechelewa kuanzishwa. Nilikuwa nategemea jambo hili lingekuja mapema sana, mara tu baada ya kuanza ujenzi wa Standard Gauge Railway. Naomba tu niseme kwamba katika bandari yetu ya Tanzania mpaka sasa hivi, pamoja na kuwa bandari yetu hii imezungukwa na nchi mbalimbali ambazo kimsingi ndio wateja wetu; Uganda, Congo, Zambia, Malawi, Mozambique, Rwanda na Burundi, tuna bahati sana.

Mheshimiwa Spika, lakini pia niseme mpaka sasa hivi katika bandari yetu ya Tanzania, uwezo wa bandari yetu kuleta makontena kwa mwaka mmoja, mwaka 2021/2022 makontena ni 820 tu ambayo yaliweza kupakuliwa kwenye bandari yetu ya Dar es Salaam, ukilinganisha na nchi ya Dubai ambako ndiko mwekezaji huyu tunayemzungumzia DP World yeye yupo na anafanya kazi, Bandari ya Dubai sasa hivi inatoa makontena 24,000,000 kwa mwaka. Kwa hiyo, mimi niseme tu kwamba wenzetu wako mbali sana.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kuwa tayari tumeshawekeza fedha nyingi sana kwenye Standard Gauge Railway, zaidi ya trilioni sita ambazo zinakwenda kuwekezwa kwenye SGR. Kwa hiyo, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kuona kwamba iko haja ya kufanya maandalizi mazuri ili kutengeneza mnyororo mzuri kwamba bandari yetu ya Dar es Salaam iweze kuongezewa uwezo na hatimaye sasa Standard Gauge Railway itakapokuwa tayari imeunganishwa vipande vyote sasa iweze kupokea mzigo kutoka kwenye bandari yetu ya Dar es Salaam na kusafirisha kwenye nchi hizo nilizozitaja.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo mimi nataka niseme kumekuwa na upotoshaji mkubwa sana. Wenzangu wamesema, lakini na mimi naomba niseme kidogo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na upotoshaji kwamba kwenye huu mkataba ambao tunauzungumzia leo hakutakuwa na marekebisho yoyote. Mimi naomba wapotoshaji hao wasifanye jambo hilo kwa sababu wanafanya kwa makusudi na wanatambua kwamba kwenye ule mkataba kuna Ibara ya 22 ambayo imejipambanua vizuri, imewekwa wazi kwamba marekebisho yoyote yanaweza yakafanyika wakati wowote.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme kwenye suala la TEHAMA; kwenye suala hili ni sehemu nyeti sana, kwa hiyo, ninashauri kwenye eneo la TEHAMA hawa wenzetu eGA wawepo, lakini pia TCRA wawepo kwa sababu mifumo hii tukiiacha iwe free kwa mwekezaji itakuwa ni hatari sana kwa usalama wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine naomba niseme, Watanzania wenzangu, Watanzania sisi kama ambavyo mnatambua mmetupa ridhaa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tuko hapa kwa niaba yenu kuhakikisha kwamba mambo yote yanakwenda vizuri na hakuna jambo litakaloharibika, kama ambavyo mlituamini tunaomba muendelee kutuamini. Lakini kama ambavyo mnamwamini Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan tunaomba pia muendelee kumwamini kwa sababu anasimamia misingi ya sheria na misingi ya utawala bora, hakuna kitu chochote kitakachokwenda tofauti.

Mheshimiwa Spika, lakini pia umoja wetu ni lazima tuuzingatie sana, tusigawike eti kwa sababu ya suala hili la bandari hii ambayo inakwenda kupata mwekezaji baada ya michakato hii yote kwenda.

Mheshimiwa Spika, naomba nimuombe sana Mheshimiwa Rais wangu, kwa kweli asitolewe kweli reli ya maandalizi na mchakato huu wa kuelekea uwekezaji mkubwa kwa Taifa hili. Wapo wanasiasa uchwara ambao wanapita kila maeneo huko kupotosha na wana kazi maalum ya kuhakikisha kwamba wanamtoa Mheshimiwa Rais wetu kwenye reli ili asiweze kusimama imara katika suala hili la uwekezaji wa bandari kama ambavyo nimezungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika wapo madalali; hawa madalali wamekuwa wakitusumbua sana katika nchi yetu na wengine ni majirani zetu tuwaombe watuachie nchi yetu tufanye shughuli zetu kwa usalama na amani kwa sababu hata wakati tulipokuwa tuna mchakato wa Ngorongoro Conservation kuhamisha wananchi kule kuwapeleka kule Tanga napo ambao waliingilia, wakaanza kuleta kelele, wakaanza kuleta vurugu. Hatuhitaji mtu yeyote aje atuingilie kwenye nchi yetu, mwacheni Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan afanye kazi yake vizuri ipasavyo na kwa vyovyote vile wanatuonea wivu kwa sababu Mheshimiwa Rais wetu yuko imara, anafanya kazi vizuri sana, amesimama vizuri sana katika kufungua masuala yote ya kiuchumi katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaaminim kabisa uwekezaji huu ukifanyika katika nchi yetu ya Tanzania maana yake tunaenda kuingiza pesa nyingi sana. Kwa hiyo, ni lazima wawe na wivu katika masuala mazima ya kiuchumi na hawa madalali wa kisiasa tunawaomba sana kama wamechukuliwa, wamelipwa fedha basi waangalie mambo yao wasiingilie masuala haya ambayo ni masuala yenye afya katika uchumi wetu wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo machache naomba nichukue nafasi hii kukushukuru na ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara ya Kilimo bajeti hii ya mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiisoma hii bejeti na maudhui yake yote ni bajeti ya kupigiwa mfano toka nimekuwa Mbunge Awamu ya Kwanza na sasa Awamu ya Pili. Kutoka Shilingi Bilioni 274 mpaka kufikia Shilingi Bilioni 751 siyo mchezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, basi niombe sasa, Mheshimiwa Waziri nia yake ni njema, amekuwa akifanyakazi vizuri sana na tunayo matumaini makubwa sana Watanzania kupitia Waziri mwenye dhamana Mheshimiwa Hussein Bashe kwa namna ambavyo amejipata vizuri yeye na timu yake kuhakikisha kwamba analeta mageuzi makubwa sana katika sekta ya kilimo. Sisi tunakutakia kila la kheri Mwenyezi Mungu akupe afya njema wewe pamoja na Naibu wako na Watendaji wako, tunamuomba tu Mheshimiwa Mama yetu Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aendelee kukuacha hapo kwenye nafasi hiyo ili malengo yako na ndoto yako ya kuwatumikia wananchi na kufanya mageuzi yatimie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumze kuhusiana na suala la mbolea. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza, kwamba tarehe 4 Aprili, katika ukumbi wa Jakaya Kikwete hapa Dodoma, Mheshimiwa Rais alizungumza na Watanzania kupitia mkutano ambao ulikuwa umeandaliwa na Waziri wa Kilimo, akaahidi kwamba katika sekta ya kilimo atahakikisha kwamba anaweka ruzuku ya shilingi bilioni 150 ili kuenda kuwasaidia wakulima kupata nafuu na afueni kwenye suala la mbolea. Ninaomba isije ikawa hapa ndani ya Bunge kazi yetu ni kudemka tu na utekelezaji haupo. Niwaombe sana Wizara ya Fedha, pesa hizi ambazo Mheshimiwa Rais amesema ziende kilimo Shilingi Bilioni 150 mkazitoe ziende na Mheshimiwa Rais anamaanisha kama hamzazijua rangi zake basi Wizara ya Fedha safari hii kama hamjapeleka fedha hii bilioni 150 mtaona rangi halisi za Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nataka nizungumzie suala la Benki ya Kilimo. Tunahitaji Benki ya Kilimo katika Mkoa wa Ruvuma. Ninaomba sana leo hii nazungumza hapa kuhusiana na suala la Benki ya Kilimo nataka nitumie lugha ya kudemka, msituchukulie kwamba kazi yetu kudemka, leo nachangia hapa nimeshauliza maswali mengi ni kama siku ya 13 ninachangia suala hili la Benki ya Kilimo, ninaomba Benki ya Kilimo ipelekwe katika Mkoa wa Ruvuma kwa sababu zifuatazo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Ruvuma ni Mkoa ambao ni Benki ya Chakula, tunawahakikishia tutashika nafasi ya tano katika uzalishaji wa mazao ya nafaka. Ni wazi kwamba Mkoa wa Ruvuma unachangia pato kubwa sana katika Pato la Taifa, linachangia fedha nyingi sana kupitia suala la kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine wakulima wangu wanalima kwa kutumia majembe ya mkono mpaka sasa hivi pamoja na kuwa tumekuwa tukiongoza na ni benki ya chakula, kwa nini Wizara ya Kilimo msitupelekee Benki ya Kilimo katika Mkoa wa Ruvuma? Tunahitaji Benki ya Kilimo na niseme Mheshimiwa Bashe kupitia hili suala la Benki ya Kilimo nimechoka kuzungumza ndani ya Bunge hili na ninakuambia kabisa ninakusudia kukamata shilingi ya yako kuzuia bajeti yako isipitishwe, endapo kama utakapokuwa unakuja hapa una-windup, huna maneno mazuri yatakayo-stimulate wananchi wa Mkoa wa Ruvuma kupata Benki ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maneno yapita yanasema kwamba ooh! Benki ya Kilimo, tumeshakopesha huko, nenda kaone wapi, tunataka iandikwe pale kama ilivyoandikwa benki nyingine Microfinance Bank tunataka iandikwe pale Benki ya Kilimo, Mkoa wa Ruvuma. Wananchi waingie pale, anayekuwa na shamba dogo la heka tano akakope, mwenye shamba la heka 10 akakope, badala ya hizo blaah! Blaa! za chini ya pazia, tunahitaji Benki ya Kilimo, unahitaji degree ngapi kujua kwamba Mkoa wa Ruvuma kuna umuhimu wa kupeleka Benki ya Kilimo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilitaka kupanda juu ya meza...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nakwenda kuchangia Bajeti ya Wizara ya Miundombinu ya Mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na Barabara ya Mtwara Pachani inayopita Luchili, Lusewa, Magazini, Nalasi mpaka Tunduru yenye urefu wa kilomita 325. Ni barabara ya mkakati, kwa hiyo, tunaomba, nimeangalia kwenye list ya barabara zile sijaona kama imetengewa pesa. Naomba sana itengewe pesa ili barabara hii iweze kujengwa na ni barabara ya kimkakati. Siku zote nimekuwa nikisimama nikihitaja hii barabara, Mheshimiwa Mbarawa sijui anaona kama sauti yangu ni nzuri sana, kwa hiyo, naimba tu, wimbo unamfurahisha lakini haitengei pesa ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Barabara Makambako - Songea yenye urefu wa kiomita 300 ambayo inahitaji ukarabati toka ilijengwa enzi ya mkoloni. Barabara hii inahitaji ukarabati, imeharibika sana. Tunaomba sana na tumekuwa tukisema sana na hata leo nimetazama hapa Mheshimiwa Mbarawa hajaitengea pesa yoyote, lakini ajue kwamba ile barabara ndiyo atakayopita kuja Songea kule, yale makorongo na yeye yanamhusu. Kwa hiyo, kwa athari ambazo zitatokea hata kwa watu wengine zitamhusu pia hata Mheshimiwa Waziri. Naomba sana hii barabara itengewe pesa ili iweze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nina mambo matatu tu. Jambo la mwisho linahusu Kivuko cha Mitomoni. Kivuko hiki cha Mto Moni ni kivuko chenye changamoto kubwa sana. Naomba unisikilize kwa makini lakini pia unisaidie pengine labda kwa sauti yako sisi tunaweza kupata pesa ya kujenga kivuko hicho cha Mitomoni ambacho kinaunganisha Wilaya ya Songea Vijijini na Wilaya ya Nyasa na kwamba ni kivuko ambacho kinaenda kuweka mkakati mzuri sana wa kiuchumi. Pia ni kivuko ambacho kinapita katika Mto Ruvuma. Kivuko hiki kimesababisha wananchi wengi sana wamepoteza maisha.

Mheshimiwa Spika, wananchi wamepoteza maisha kwa sababu Mto Ruvuma una mamba wengi sana na kwamba wanatumia magome ya miti ili kuvuka, hakuna kivuko. Wakati fulani Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Nyasa na Jimbo la Peramiho wamejitahidi sana kufuatilia lakini nami nataka niseme kwa mara nyingine tena. Mheshimiwa Naibu Waziri Kesekenya mwaka jana ambapo watu watano walipoteza maisha kwenye kile kivuko nilimfuata na nikampa simu akaongea na wananchi ambao wamepoteza familia zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata alivyozungumza nao, bado hakuona uchungu wala hajaona huruma na wala hajatenga pesa kwa ajili ya kwenda kujenga kivuko hicho. Nataka nikusomee watu ambao wamepoteza maisha kwenye kile kivuko, inatia huzuni, inatia huruma, watu wale ni wananchi wa Tanzania. Tunapolalamika hapa inaonekana kama vile sijui ni ng’ombe tu au ni wadudu gani? Hawa ni binadamu ambao wana haki ya kuishi, lakini tunalalamika kwamba kivuko pale hakitengenezwi na hakuna hatua zinazochukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kivuko hata kama kingetengenezwa cha muda cha shilingi Milioni sita kingesaidia kuokoa maisha ya wananchi wale. Milioni sita wanataka kuniambia Wizara hii haina milioni sita ya kujenga kile kivuko?

Mheshimiwa Spika, nataka nikutajie uone kwanza nachangia huku natetemeka namna ambavyo wananchi wamepoteza maisha. Nakutajia mwaka 2016 wananchi tisa walipoteza maisha kwenye kile kivuko. (Makofi)

MHE. ENG. STELLA MNYANYA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Stella Manyanya.

MHE. ENG. STELLA MNYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, dada ungeniacha tu nitiririke leo jamani. (Makofi/Kicheko)

TAARIFA

MHE. ENG. STELLA MNYANYA: Mheshimiwa Spika, pamoja na jithada ambazo zimeshafanyika za kufanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya kujenga daraja la kudumu katika Mto huo Ruvuma. Kwa kweli naungana na mdogo wangu kuomba sana angalau kipindi hiki tunachosubiri, basi tupate hicho kivuko.

SPIKA: Mheshimiwa Manyanya hiyo siyo taarifa. Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, naomba unilindie dakika zangu. Mwaka 2016 watu tisa walipoteza Maisha; Zulfa Mtauchila, Awetu Mohamed, Fadhili Hamis, Rajabu Said, Bahati Mustafa, Khadija Said, Seleman Abdallah, Said Waziri, Omary Mohamed. Hao walipoteza maisha mwaka 2016, Wizara inajua watu hawa wamepoteza maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2017 Omary Bandawe alikuwa anavuka anaendesha mtumbwi, mtumbwi ule ulipinduliwa na mamba akatumbukia huko na hakuonekana mpaka kesho. Mwaka 2017 hiyo hiyo Wizara inajua ndugu Omary Chinguo nae alipoteza maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, 2021 mwezi Mei tukiwa kwenye Bunge la Bajeti, Mheshimiwa Waziri anajua watu saba walipoteza maisha kwenye kivuko kile kile. Mimi leo sipandi juu ya meza, lakini nataka niseme hawa ni Watanzania wanahaki ya kuishi. Niruhusu nipige magoti kuomba kivuko kile kikajengwe. Tafadhali sana naomba kivuko kile kikajengwe kwa sababu wananchi hawa ni Watanzania na wana haki ya kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba leo nitaondoka na mshahara wa Waziri, sitaurudisha na siungi mkono hoja. (Makofi)

SPIKA: Haya ahsante sana. Sasa Mheshimiwa Ngonyani ulivyotoka tu hapo kwenye kiti chako ukaenda kupiga magoti yote uliyoyasema yale hayajaingia kwenye Taarifa Rasmi za Bunge.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, naomba, napiga magoti leo hii. Siungi mkono hoja, siungi mkono hoja leo hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia Wizara hii ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ambayo inahitaji shilingi bilioni 44. Kwa uchache tu kwamba hii shilingi bilioni 43 kwa Wizara hii nyeti kabisa bado ni ndogo sana sana, ilitosha tu iongezeke. Nilikuwa natarajia kwamba Wizara hii ije na maombi ya kuanzia shilingi bilioni 800 huko shilingi bilioni 900 kama Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, jukumu la kulea watoto wetu ni la kwetu sisi wenyewe kama wazazi, lakini pia wamesema Wabunge wengine kwamba mtoto kama mtoto hawezi kujisemea mwenyewe. Ni dhahiri shahiri kwamba mtoto anaweza akakosa hata lishe, lakini asiseme, hata kama anahitaji mahitaji maalum bado akashindwa kusema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakumbuka nikiwa mdogo enzi ya Mwalimu nchi yetu ikiwa bado changa sana na ni masikini lakini wazazi wetu walikuwa wakienda kwenye masuala ya kliniki watoto wanapopimwa wanapoondoka walikuwa wanaondoka na maziwa ya unga, walikuwa wanaondoka na mkate vitu kama hivyo.

Sasa mimi naomba Wizara hii pia mama yetu Dkt. Gwajima hebu iboreshe hii Wizara na vitu kama hivi viweze kufanyika at least kuwe na motisha kwa mtoto, hata ikifika tarehe ya mtoto kwenda kliniki mtoto mwenyewe wakati mwingine mwenye umri wa miaka mitatu/minne akaweza kukumbusha. Waweze kupata motisha mbalimbali kama maziwa, blueband na nini na mambo mbalimbali. Hata hivyo ninaamini kabisa wewe ni jembe kweli kweli, unaweza ukaandika na maandiko na nini Wizara yako ikaendelea kupata misaada kama hiyo na ikaenda kutolewa kwenye zahanati na vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liko jambo ambalo liko kwenye jamii yetu ambalo limejitokeza sana, wako baadhi ya wanaume/akina baba, wanadhulumu haki za watoto kwa kunyonya maziwa ya mama ambayo mtoto ndio alipaswa anyonye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili limejitokeza katika mikoa mbalimbali niombe Wizara ifanye utafiti yako majibaba yanafakamia maziwa ya watoto wanawanyonya wale wake zao wanaonyonyesha. Badala ya mtoto anyonye maziwa yale na kupata ile lishe basi baba anakwenda ananyonya; na kuna mtu ameniongezea nyama hapa akaniambia hivi kwamba yale maziwa ya mama kwanza yana virutubisho sana wako baadhi ya akina baba wamegundua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia yale maziwa ya mama yanasaidia kukata hangover ya walevi ambao wanakuwa wamekunywa pombe na yanasaidia kukata hiyo hangover. Kwa hiyo, niombe sana Wizara iweke mpango mzuri na itoe elimu ili akina baba hawa wasiwadhulumu watoto haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie pia suala la kisiasa; kumekuwa na ukatili mkubwa sana wa kijinsia kwenye masuala ya kisiasa kwa wanawake ambao wanachipukia kwenye masuala ya siasa, hususan hata sisi Wabunge wanawake humu ndani, tumekuwa tukinyanyapaliwa kwenye maeneo yetu tunapofanya shughuli zetu za kisiasa. Kwa hiyo, huu ukatili Wizara imejipangaje kuhakikisha kwamba inatusaidia sisi wanawake tunaokua kisiasa kwenye maeneo mbalimbali, ili tuweze kufanya shughuli zetu za kisiasa bila kufanyiwa ukatili, ikiwemo ukatili wa kwenye mitandao?

Mheshimiwa Spika, maana Mbunge mwanamke anaweza akasema jambo hapa na Mbunge mwanaume akasema jambo hilo hilo, lakini utakuta Mbunge mwanamke ananyanyapaliwa kwenye mtandao, anatukanwa matusi makubwa makubwa ya nguoni. Tunaomba Wizara muone namna gani ya kusaidia jambo hili ili lisiendelee kujitokeza kwa sababu, sisi sote ni Watanzania na ni jamii moja.

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie ukatili wa kingono…

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: …jamani naombeni leo sina… Naomba Taarifa kaeni nazo, leo hii naomba. Nina mambo mahususi sana hapa. Nina jambo mahususi sana la kuchangia. Tafadhali kaka yangu nakuheshimu, nakupenda sana. (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ramadhan Ramadhan.

T A A R I F A

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe Taarifa mzungumzaji, mama yangu kwamba wako wasichana na wanawake wengi wamekata tamaa kuendelea na shughuli za siasa kwa sababu ya unyanyapaa anaoendelea kuusema. Kwa hiyo, naomba nimpe Taarifa kwamba, hilo tatizo kweli ni kubwa na lazima hatua zichukuliwe. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naipokea sana, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nizungumzie ukatili wa kingono; Wabunge wenzangu wengi wamechangia hapa kuhusiana na ukatili wa kingono kwa wanawake. Ni kweli kabisa ukatili wa kingono katika nchi yetu ya Tanzania umeshamiri sana, lakini mimi nitaliongelea jambo hili kitofauti kidogo.

Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya UKIMWI na kwa kuwa ni Mjumbe wa Kamati ya UKIMWI, nitazungumza jambo ambalo linahusiana na suala la maendeleo ya jamii, lakini pia nitahusianisha na suala la ngono ambalo linaungana pia na suala la UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, hapo unanipoteza unaponyanyua nyanyua microphone, naona kama unataka unikatishe. Naomba sana tafadhali.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja, malizia.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, dakika moja.

Mheshimiwa Spika, wako wanaume ambao hawataki kufanya tohara na kwa misingi hiyo wanataka kuwaingilia wanawake kwa maana ya kuwapa huduma hiyo bila kufanya tohara. Sasa mimi nitoe wito kwa Watanzania wote wanawake wenzangu kwamba suala la mwanaume ambaye hajafanya tohara kushirikiana naye ni hatari kwa afya yako na niseme tu kwamba inasababisha saratani ya shingo ya kizazi. Kwa hiyo, haifai kabisa kwa matumizi ya binadamu na wakatae kutoa huduma hiyo endapo kama atamkuta mwanaume hajafanyiwa tohara kwa sababu inasababisha saratani ya shingo ya kizazi. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
The Finance Bill, 2016
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Muswada wa Sheria ya Fedha 2016. Nimefurahi sana baada ya Serikali kuona umuhimu wa kukusanya kodi ya majengo na kutokuziachia Halmashauri zetu ziendelee kukusanya. Ni wazi kwamba hata wenzangu watakuwa ni mashahidi pesa nyingi sana zilikuwa zinapotea zilizokuwa zinatakiwa kukusanywa kwenye majengo hasa zilipokuwa zinakusanywa na Halmashauri, kwa sababu Halmashauri zetu zilikuwa zinatumia utaratibu wa kuweka wazabuni ambao wanakusanya pesa. Kimsingi wazabuni ndiyo walikuwa wananufaika na kuziacha Halmashauri zetu zikiwa mbavu za mbwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kidogo kwenye eneo hili kwa maana ya maboresho, ukiangalia katika marekebisho haya namna ambavyo nimeona kwenye ukurasa wa nne, kipengele cha sita imeeleza bayana kwamba TRA ndiyo itakayokwenda kukusanya hizi pesa. Pesa hizi zitakapokuwa zimewekwa kwenye Mfuko Maalum mwisho wa siku zitarudishwa kama zilivyo kwenye miji yetu kama ilivyokuwa imeanishwa au kwenye Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo hili naomba niseme yafuatayo:-
Ukiangalia katika miji mikubwa mfano Mji wa Dar es Salaam, ni mji ambao unakua kwa kutegemea michango ya kodi za maendeleo kutoka katika Mikoa mbalimbali ya Pembezoni. Mikoa ya pembezoni ni watu ambao wanakusanya kodi kupitia aidha kilimo, wengine kwa shughuli nyinginezo. Kwa Mkoa wetu wa Ruvuma, wakulima wa korosho, tumbaku pamoja na mahindi ndiyo ambao wamekuwa wakichangia hata ikafikia Mkoa wa Dar es Salaam sasa unaweza kuwa na miundombinu mizuri. Kwa mfano tunajenga fly over, lakini pia tumejenga daraja lile la Kigamboni pamoja na barabara zilizopo katika Mkoa wa Dar es Salaam na miradi mingine yote mikubwa inajengwa pale kwa sababu ule ndiyo Mji Mkuu wa Tanzania, kwa hiyo, lazima uwe na sura nzuri ambayo inavutia wawekezaji kwenda kuwekeza katika Jiji la Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kodi hizi zinazokusanywa kutoka katika maeneo mbalimbali kwenye mikoa yetu ndiyo zinawezesha Jiji la Dar es Salaam kupata wawekezaji wengi na kuonekana kwamba, Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam ndiyo zitakusanya pesa nyingi sana kwenye maeneo haya ya kodi ya majengo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukusanya pesa hizo wao wataendelea kustawi, Halmashauri zao zitaendelea kustawi, wakati Halmashauri zingine za pembezoni zitakuwa zinasinyaa kwa sababu zenyewe chanzo chao cha mapato kinategemea hasa kilimo na miundombinu yake bado haijawa wezeshi ili kuwezesha aidha kuweka viwanda, aidha kuvutia wawekezaji wa aina mbalimbali kuja kuwekeza kwenye maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sasa Serikali ifanye yafuatayo kwa maana ya ushauri wangu. Nadhani kwamba baada ya TRA kukusanya pesa na zikawekwa kwenye Mfuko, basi pesa zile zikagawiwe sawa kwa sawa kwenye Halmashauri mbalimbali katika nchi yetu, ili kuziwezesha Halmashauri nyinginezo ambazo zina hali duni, ziweze na zenyewe kuchipua, ziweze kufikia hatua ambayo itawavutia wawekezaji kwenda kuwekeza kwenye maeneo yao, kwa sababu tayari wataweza kutengeneza miundombinu ambayo itakuwa wezeshi na miundombinu ambayo itakuwa ni kivutio kwa wawekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nisisitize sana kwenye eneo hili, ukizingatia katika Wilaya yangu ya Tunduru, wamekuwa wakizalisha na pato kubwa sana linatokana na zao la tumbaku, halikadhalika Namtumbo wamekuwa wakizalisha tumbaku, wanapata pato kubwa sana ambayo inawezesha katika Serikali hii, lakini pia hata wenzetu wanaolima mahindi Songea Mjini, Songea Vijijini nao pia wamezalisha sana kupelekea hili pato kuendelea kukua na kuendesha mikoa mingine. Halikadhalika…
NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa…
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Nakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Spika, haya yakizingatiwa itapendeza sana. Naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Muswada wa Sheria wa Upatikanaji wa Habari wa mwaka 2016.
Pia nichukue nafasi hii kuwapongeza sana wenzetu Kamati ya Katiba na Sheria ambao waliona umuhimu wa kuleta sheria hii ili tuweze kuichanganua kadri tutakavyoweza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, naomba pia niwapongeze sana wadau wote walioshiriki kuchakata sheria hii wakiwemo Chama cha Wanasheria, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, Sekretarieti ya Msaada wa Sheria, Baraza la Habari Tanzania na wadau wengine wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba ni jambo jema sana ambalo limeletwa kwetu kwa misingi ya kwamba kutokana na hali halisi juu ya upatikanaji wa habari ambao umekuwa ukiendelea katika nchi yetu, kumekuwa na haja kubwa sana ya kuleta sheria hii na kuweza kuifanyia marekebisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa habari sasa hivi katika nchi yetu umekuwa ni wa kiholela tu, kila mtu anajiamulia kadri anavyoweza na anaweza akaamua tu akaanzisha habari yoyote ile isiyokuwa na uhakika; lakini pia Taifa letu tayari limeshaingia kwenye hali ya kuwa kila siku kunakuwa na habari zinaibuka na hatimaye tunakuwa na kazi ya kukanusha kanusha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachelea kusema habari ambazo zinakuja kinyume na utaratibu ambazo hazijahakikishwa na hatimaye kutolewa, unaweza kusema ni sehemu ya umbea tu. Kwa sababu imeonekena kwamba habari nyiungi sana za kulipuka zinatupiwa kwenye magazeti, zinawafanya watu waweze kuuza magazeti tofauti na hali halisi ambayo inatakiwa iende. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii itakwenda sasa moja kwa moja kumbana mtoa habari. Itakwenda kumbana mtu ambaye anayekwenda kutoa taarifa ambayo siyo. Kwa mfano, labda niseme tu, siyo muda mrefu kama mwezi mmoja na nusu au miwili imepita, nadhani wenzangu watakuwa mashahidi, kulikuwa na habari ambayo ilitupiwa kwenye mtandao kwamba Jerry Muro amekuwa ni Kaimu Mkurugenzi Ikulu, lakini ni jambo ambalo lilikuwa siyo la kweli. Hatimaye akasema kwamba amekuwa Kaimu Mkurugenzi na Greyson Msigwa amekuwa Mkurugenzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hizi zilikuwa siyo za kweli, badala yake sasa Serikali ikaanza kufanya kazi ya kukanusha jambo hilo. Sasa hatuwezi kuwa na Taifa ambapo kila siku ni kupeleka habari, mtu anaamua tu; kesho yake mtu anaanza kukanusha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ni jambo ambalo kimsingi limempata dada yangu Mheshimiwa Magdalena Sakaya. Leo hii mmeshuhudia yeye mwenyewe anakanusha hapa. Wameshatengeneza habari kwamba amefukuzwa Chama cha CUF, jambo ambalo siyo kweli.
Kwa hiyo, tutakapokwenda kuitengeneza hii sheria na tukaiweka sawa sawa, itakuwa inasimama pande zote mbili; hakuna ambaye ataathiriwa na Sheria hiyo. Endapo tu kama mtu ataona yeye anahitaji kufanya hivyo, basi atakuwa ameamua yeye kwa makusudi na sheria itakuwa inachukua mkondo wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nataka tu niwakumbushe wenzangu; juzi tumepata habari nyingine, eti Makamu wa Rais anataka kujiuzulu. Yaani ni mtu ameibuka tu anaanzisha kitu from no where. Kwa hiyo, 81
nadhani hii sheria ni vizuri tukaenda kuipitisha wote kwa pamoja ili kuepuka vitu ambavyo mtu anaweza akaibuka tu akajifanyia bila sababu za msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeshuhudia juzi hapa tunaambiwa kwamba Mheshimiwa Freeman Mbowe ametolewa vitu vyake National Housing, jambo ambalo halina ukweli kwa sababu yeye mwenyewe amekuja amekanusha. Eti kwamba anadaiwa shilingi bilioni 1.6. Amekanusha na akasema kwamba anaenda mahakamani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sheria hii tukiisimamia vizuri, itacheza pande zote mbili ili kuwafanya watu katika nchi yetu tusiwe na ile hali ya kulipuka, kila mmoja anaamua from no where tu, mtu aanzisha habari yake, halafu tunarudi kwenda kukanusha; na tuone hii adha kwamba, badala ya kufanya shughuli nyingine basi tunaanza kuingia kwenye shughuli za kukanusha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba naomba nikubaliane na kipengele ambacho kinasema, Sheria ya Usalama wa Taifa isiguswe. Mtu akitoa taarifa upande wa Usalama wa Taifa, mimi nikubaliane na kipengele hiki kwa Sheria ya mwaka 1970, chini ya Ibara ya (6) kwamba mtu huyu kwa kweli achukuliwe hatua za kisheria na aweze kufungwa miaka 15.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye amendment kwamba imefanyiwa marekebisho, badala ya kiama 20 na 15, basi mtu anaweza akafungwa kifungo cha miaka mitatu mpaka mitano. Mimi napendekeza miaka 15 na 20 ibaki pale pale badala ya kupunguzwa. Kwa sababu watu wengine watafanya kwa makusudi. Anakwenda kwa makusudi kutoa taarifa za usalama wa nchi ili nchi yetu iingie kwenye janga kubwa; na watu wengine wako tayari hata kujitoa mhanga. Kwa hiyo, miaka mitatu au miaka mitano ni kitu kidogo sana. Naomba kama inawezekana, hili jambo libaki pale pale na hii adhabu ibaki pale pale kwa maana ya miaka 15 mpaka miaka 20.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nichukue nafasi hii kumshukuru pia Mwenyezi Mungu kwa namna ambavyo imefika mahali ambapo sisi na wenzetu watani wetu tuko pamoja humu ndani. Ni jambo ambalo niseme tu wenzetu hawa tuliwa-miss sana na waliporudi sisi tuna amani na kimsingi wao wenyewe waliamua kuziba na baadaye wamezibua wenyewe.
Karibuni sana ndugu zetu, tuendelee kuchakata hizi sheria ili tuendelee kuwa pamoja, tuendelee kushirikiana kwa mustakabali wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, naomba kuwasilisha.
Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo, wa Mwaka 2016
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye amenijalia kusimama hapa siku hii ya leo. Pia nakushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii adhimu ili nami niweze kuchangia Muswada wa Sheria ya Kuanzishwa Taasisi ya Kilimo ambayo inaitwa TARI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maoni yangu, nashauri kwamba Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa pamoja tukubaliane ili tuweze kupitisha sheria hii iweze kuanza kufanya kazi ili watafiti waweze kunufaika na sheria hii.
Lengo la Muswada huu, kwa maana ya sheria hii ni kusimamia tafiti zote za kilimo Tanzania nzima. Kwa kuwa sheria hii ilikuwa haijaundwa, basi ilikuwa inapelekea, watafiti wanapoanzisha utafiti, mwisho wa siku wanashindwa kufika mwisho na utafiti ule ulikuwa hauzai matunda yoyote. Kwa hiyo, ulikuwa haumnufaishi mwananchi wetu wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme tu, utafiti uliokuwa ukifanywa ulikuwa siyo mzuri kiasi ambacho kwenye maeneo mbalimbali tumeshuhudia. Kwa mfano, katika Mkoa wetu wa Ruvuma, mbegu ambazo zimeletwa kwa maana ya uzalishaji wa mahindi ni mbegu za ajabu sana. Unashangaa kuona kwamba mhindi unakuwa kufikia futi moja na nusu eti ndiyo unachanua. Sasa huo muhindi unaochanua hivyo ni wazi kwamba unakwenda kubeba kipande cha mhindi kidogo sana. Kwa hiyo, hizi mbegu nyingi ambazo zimekuwa zikiletwa kwetu siyo nzuri, hazifai. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nadhani kwa kufanya maboresho na kwa kupitisha sheria hii sasa itakwenda kuhakikisha kwamba tunapata watafiti ambao watakwenda kufanya utafiti mzuri na kuweza kuongeza mapato katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado pia imeonekana kwamba Maafisa Ugani wapo tu jina, hawana kazi yoyote ambayo wanaifanya ya kuweza kuboresha mazao katika maeneo yetu ambayo tunaishi. Wapo wapo tu, wanapokea mishahara lakini kazi zile za msingi sisi hatuzioni. Kwa sababu kama mbegu ya mhindi inaletwa inafikia futi moja halafu inabeba mtoto pale; ni sawa sawa hata sisi akinamama, mwanamke ambaye anaweza akatotoa mtoto mzuri kweli kweli ni yule ambaye angalau anakuwa na urefu kiasi fulani, ingawa hata yule mfupi anaweza akatoa mtoto ambaye anafaa; lakini niseme tu kwamba mbegu ambayo inakuwa imekua kwa maana ya mahindi, ndiyo ambayo inaweza ikabeba mtoto mzuri. (Minong’ono)
Mheshimiwa Mwenyekiti, samahani sana, sina maana mbaya kwa wale wafupi, ni kwa ajili tu ya kuchambua ili nieleweke kwenye eneo hili la suala la mbegu. Tupo pamoja, naomba Waheshimiwa Wabunge wasinielewe vibaya. (Makofi/Kelele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na Maafisa Ugani, Maafisa Kilimo na wenyewe wapo lakini hizi mbegu zinakuja feki hawasemi chochote, wapo tu wamekaa. Kwa hiyo, suala la utafiti ni muhimu, naomba tupitishe hii sheria ili tuweze kupata mazao mengi na mazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme faida ya kuhakikisha kwamba tunapitisha hii sheria, maana yake, uzalishaji utaongezeka. Pia teknolojia mpya dhidi ya kilimo zitagundulika kutokana na utafiti huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye Taasisi ya Uvuvi kwa maana ya TAFIRI. Hapa kwenye suala la uvuvi utafiti huu utasaidia kuongeza uzalishaji wa viumbe hai kwenye mito, maziwa au bahari. Ni utamaduni ambao umezoeleka, watafiti wetu mara nyingi sana walikuwa wanajikita kwenye bahari na kwenye maziwa, lakini sijaona watafiti wanafanya utafiti wa uzalishaji wa samaki kwenye mito; sijaona watafiti wamejikita kisawasawa kwenye uzalishaji wa samaki kwenye mabwawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watafiti wakijipanga vizuri, zao la uvuvi wa samaki linaweza likatusaidia kwa asilimia kubwa sana kuinua kipato katika nchi yetu. Niseme tu, kule kwetu huwa tunachimba na visima hivi vya maji; lakini unaona kisima wamekichimba kienyeji tu, baada ya miezi mitatu ukienda kusafisha unakuta kambale wamejaa kibao. Hivi hawa kambale, au hawa watafiti wetu hawawezi kuingia huko wakafanya utafiti wa kina wakatengeneza mazingira, hatuwezi kupata samaki wengi jamani? Hatuwezi kuinua kipato! Kwa hiyo, niseme tu huu utafiti na hii sheria tukiipitisha, itakwenda kuwasaidia watu wetu wafanye utafiti wa kina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ile mito iliyopo; Tanzania tunasema ni nchi tajiri ambayo ina mito na mabonde. Mito mingine jamani kwa haki ya Mungu imeamua tu sasa ijikaukie tu, kwa sababu hakuna jambo lolote linalofanyika dhidi ya hiyo mito, ipo tu. Zipo nchi ambazo, yaani mtoto anatolewa darasani kupelekwa kwenye mto ili awe kama anatembelea mto aone unafananaje; lakini huku kwetu hatua 20 mto, ukienda kilometa ngapi, mto; lakini ile mito imekaa tu, haifanyiwi utafiti wowote, hakuna kitu chochote ambacho inazalisha, mwisho wa siku inaamua ijikaukie tu. Nao uumbaji wa Mwenyezi Mungu kama huutumii, basi inaamua ijikaukie tu. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani sheria hii tukiipitisha itaongeza mazao katika suala la uvuvi, lakini pia itaongeza kipato na itaongeza lishe. Pia niseme, mimi sio daktari, lakini utafiti umeonesha kwamba samaki anaongeza afya nzuri sana, lakini pia inasaidia hata ukuaji wa ubongo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukilalamika hapa tunasema watoto wengine hawana afya bora, nadhani kama tutaboresha na watafiti wetu wakafanya utafiti wakaona ni samaki wa aina gani, kama tukiwatunza vizuri, tukaona labda katika Nyanda za Juu Kusini kwamba ni samaki wa aina gani wazalishwe; haya, wakaenda labda kwa mfano, kwenye centre hii tuliyopo hapa Dodoma ni samaki wa aina gani wazalishwe ili samaki hawa sasa wawe wanazalishwa kila maeneo kwa ajili ya kusaidia lishe, hasa kwa watoto wetu ambao ndiyo tunatarajia kwamba ndiyo zao la watoto wetu wanaoanza sasa waweze kupata samaki wale, ili waanzie hapo sasa kuboresha afya zao na kukuza vizuri kwa ufasaha zaidi ubongo wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu tunachokihitaji siyo tu uwezo wa kufaulu darasani, lakini tunataka mtoto mwenye akili ambaye anaweza akafanya utafiti mzuri kwa kutumia ile akili yake. Kwa hiyo, kama ukitaka tu kwa kufaulu, mtu mwingine anaweza akachungulia kwa mwenzake akafaulu. Tunataka watoto ambao kweli wana afya bora kwa kupitia huu uzalishaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani pia katika sheria hii iundwe panel ili iweze kwenda kusaidia kuwasimamia hao watafiti watakaokuwa wanaenda kufanya utafiti. Badala ya kujifanyia utafiti tu kiholela, ikafika mahali mtu ameshapiga mpunga wake, ameweka mfukoni, hana haja ya kuendelea na utafiti, anasema tu kwamba nimeishia hapo na wala hakuna sheria ambayo atachukuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme hii panel itakayokuwa inasimamia itatazama mwenendo wa wale watafiti, mwisho wa siku kabla hawajamaliza utafiti wao, wanaweza wakafikia nusu na wakaambiwa kwamba kwa utafiti wenu huu, tumeona kwamba hamtoshelezi na…
MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri.
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (no. 2) Act, 2022
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu kuhusiana na Muswada huu wa Sheria kwa marekebisho haya kwenye eneo la usafirishaji wa binadamu lakini pia dawa za kulevya.

Mheshimiwa Spika, jopo letu la wanasheria katika Kamati ya Katiba na Sheria tumekaa tukajadiliana kwa makini sana; na kimsingi tumekubaliana na mapendekezo ya Serikali juu ya suala linalohusiana na marekebisho ya sheria hii, Ibara ya 9(13) na Sheria ya Dawa za Kulevya, kwamba yanafanana kabisa na Sheria ya Usafirishaji wa Binadamu. Haya yanaitwa ni makosa ya Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, ambao wanahusika moja kwa moja kwenye suala la usafirishaji wa binadamu na dawa za kulevya ni matajiri wakubwa sana ambao kimsingi wao wanapata fedha lakini athari kubwa sana inakuja katika jamii ambao ni masikini. Watu wa mwisho ndio ambao wanakuja kupata athari kubwa sana, ikiwepo makundi ya vijana, wanawake pamoja na watoto.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuhusiana na suala la usafirishaji wa binadamu Kamati imekaa na imekubaliana na kifungo hicho. Na mimi nasema, ni vizuri basi sheria hii ikatiliwa mkazo ili wasafirishaji hawa wanaofanya biashara hii ya usafirishaji wa binadamu waweze kupata kifungo cha Maisha. Sambamba na kifungo cha maisha mahakama ipate nafasi ya kuongeza kifungu cha kutoa faini, ambayo ni Shilingi milioni 100 au Shilingi milioni 200.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo nilikuwa nataka tu nitoe ufafanuzi ili kutoa uelewa kwa nini tunazungumzia suala la usafirishaji wa binadamu. Ni kwamba, suala hili halifai na tunalipiga vita sana, na ndiyo maana imeletwa sheria hapa ili kuweza kurekebisha katika vifungu hivyo na kutia mkazo.

Mheshimiwa Spika, kimsingi binadamu anaposafirishwa kwenda kwenye maeneo mbalimbali maana yake wanakwenda kutumika visivyo wakati mwingi tumeona kwamba kuna malori yanapita ndani ya nchi yetu yakisafirishwa kwenda kwenye maeneo mengine tunakuta kuna binadamu pengine zaidi hata ya 200 wamepoteza maisha, wamefia humo kwenye malori.

Mheshimiwa Spika, pia wapo wafanyabiashara wa usafirishaji wa binadamu ambao kimsingi wanachukua binadamu wanawadanganya kwamba labda pengine wanakwenda kupata ajira sehemu, hususani mabinti na wanawake. Wanawaambia kwamba tunakwenda kuwapeleka huko na mtapata kazi nzuri mtapata ujira mkubwa. Mwisho wa siku wanakwenda kuwatumia kwa masuala mbalimbali ikiwepo masuala ya madanguro; wanatumika vibaya huko, lakini pia wamekuwa wakipoteza maisha. Hii pia inaambatana na biashara ya viungo vya binadamu. Kwa hiyo kumekuwa na athari kubwa sana katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi napendekeza pia kwamba sheria kali hii itiwe mkazo kupitia Bunge lako Tukufu ili suala hili liweze kukomeshwa mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na dawa za kulevya; kifungu Na. 32(5) kimeletwa katika Bunge hili kupitia Kamati ya Bunge, lakini pia Serikali ili kiweze kufanyiwa marekebisho. Sisi kama Kamati tumeshauri kwamba ijengwe mahabusu maalum kabisa ambayo itashughulikia suala la hawa mahabusu wanaohusiana na dawa za kulevya. Nimeona hapa kuna hoja mbalimbali, taarifa na nini, lakini kimsingi niseme tu kwamba, mahabusu hii inajengwa kwa makusudi kabisa ili iweze kutoa wigo mpana wa taasisi maalum kushughulikia suala hili kwa ukaribu na kwa ukamilifu zaidi bila kuathiri tendo lenyewe la kushughulikia suala hili.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, hawa wenzetu ambao wanashughulika na dawa za kulevya wamekuwa wakihitaji zaidi kupanua masoko yao. Endapo wanakutana na makundi ya watu wawili watatu basi ni fursa kwao kwa ajili ya kutoa elimu dhidi ya dawa za kulevya na kuhamasisha suala hili liweze kuendelea na kukua zaidi. Kwa misingi hiyo, endapo muuzaji wa dawa za kulevya anakamatwa anahusishwa kwenye mahabusu ya raia wengine wakiwepo pale polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mahabusu haichagui, maana yake mwizi wa kuku atakuwa humo, mwengine amebishana tu jirani yake atakuwa humo, wengine wana makosa madogo ya udokozi watakuwemo humo. Sasa anapoingia gwiji huyu wa dawa za kulevya kwenye mahabusu hiyo ya polisi ni wazi kwamba atatoka mle ameshafanya kazi yake ya kuwaelimisha na kuwahamasisha waliomo mle waondokane na wizi wa kuku, udokozi na uvutaji wa bangi na mambo mengine. Badala yake sasa waingie kwenye biashara ya dawa za kulevya kwa kuwahamasisha kwamba biashara hii inalipa na kwamba wanaweza Kwenda kuwasaidia kupata uwezeshaji ili nao waweze kusafirisha madawa hayo ya kulevya.

Mheshimiwa Spika, na mtu akishawishiwa kwenye maeneo hayo anakubali, anaona kwamba kama mnaiba kuku na nimefikia hapa je, nikisafirisha dawa za kulevya maana yake atapata pesa nyingi. Kwa hiyo kuwakutanisha na wale watu wa aina hiyo kunatoa fursa kwa wauzaji wa dawa za kulevya kushawishi jamii nyingine ambayo sasa hatimaye inaingia kwenye janga hilo.

Mheshimiwa Spika, mimi nataka nizungumzie pia dawa ya kulevya aina ya bangi. Pamoja na kukaa na jopo la wanasheria wenzangu ndani ya Kamati lakini mimi nimetoka pale nikiwa niko tofauti kabisa na wanasheria wenzangu. Mimi nitaizungumzia bangi kivingine kabisa leo tofauti na ambavyo tumezungumza kwenye Kamati.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunaweza tukahangaika na cocaine tukahangaika na heroine ambayo kimsingi hatuizalishi katika nchi yetu hapa, inakuja kutoka katika nchi nyingine. Tumekuwa tukihangaika kuziba mipaka na kununua vifaa vingi vikubwa vya gharama kubwa kwa ajili ya ku-sense hayo madawa ili hatimaye tuweze kubainisha madawa hayo na kuhakikisha kwamba tunayatokomeza. Lakini bado tatizo lipo na ndugu zetu, wananchi wenzetu wanaendelea kuteseka na hizi dawa na athari kubwa imeendelea kusambaa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sasa ukiacha cocaine, heroin na dawa nyingine zinazofanana na hizo, suala la bangi mimi naona ndilo tatizo kubwa sana, kwa sababu bangi inalimwa hata kwenye upenuni mwa nyumba, hata bafuni mtu anaweza akaiweka bangi hiyo na ikalimwa hapo na kwamba mtu ataibembeleza mwisho wa siku anavuta kimya kimya. Hatuna vifaa ambavyo vita-sense kwamba nyumba hii kuna bangi, shamba hili lina bangi.

Mheshimiwa Spika, sasa basi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja malizia.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Maoni yangu; kwa nini suala hili la bangi tusilichukue tukakaa upya tukajadiliana ili ikiwezekana bangi hii tui-process na tuweze kujenga viwanda ambavyo vitapunguza makali ya ile bangi ili bangi hii iweze kutumika kwenye maeneo mbalimbali? Kwa sababu wako watu wakitumia hivyo wanaweza kulima zaidi anaweza kufanya hii na mwingine anavuta tu kama sigara. Pia nitoe mfano kuna nchi ya Zimbabwe wanalima bangi na tayari wameshaipitisha na ni biashara inaingiza Pato la Taifa. Jamaica, Marekani, Korea Kaskazini kwa nini sisi tusi-process tukapunguza makali na hatimaye watu wakaitumia kadiri mtu anavyoona. Sawasawa na sigara wanasema tumia lakini ni hatari kwa binadamu wameweka caution pale, kwa hiyo mtu ana hiari kuitumia au kuiacha, kuliko kuacha Pato hili la Taifa linaendelea kutokomea wakati watu kila nyumba na katika maeneo mbalimbali wanaendelea kuitumia hii bangi na hatuna vifaa vya ku-sense hiyo bangi kuibaini.

Mheshimiwa Spika, asante sana naomba kuwasilisha. (Makofi)