Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Juliana Daniel Shonza (26 total)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU aliuliza:-
Uandaaji wa Mashindano ya Kimataifa ya Mpira wa Miguu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu la Afrika (CAF) unataka Miji miwili iteuliwe kuendesha mashindano hayo:-
Je, Serikali imeteua mji upi wa pili mbali na Dar es Salaam kuendeshea Mashindano ya AFCON ya vijana chini ya umri wa miaka 17 ya mwaka 2019 yatakayofanyika Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa sababu leo ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako Tukufu, naomba kwanza nichukue nafasi hii kuweza kumshukuru Mwenyezi Mungu. Kwa kipekee kabisa nichukue nafasi hii kuweza kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Magufuli kwa imani yake kubwa ambayo ameionesha kwangu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kipekee kabisa nikushukuru wewe mwenyewe Naibu Spika pamoja na Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mchango wenu na ushirikiano wote ambao mlikuwa mkinipa kipindi nikiwa Mbunge. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako pia naomba nichukue nafasi hii kuweza kuwapa pole wazazi, wanafunzi pamoja na Walimu wa Nduda iliyopo katika Mkoa wangu wa Songwe kwa kuondokewa na wanafunzi ambao walifariki baada ya kupigwa na radi wakiwa shuleni. Nawaombea Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi. Amina.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Elibariki Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, uteuzi wa maeneo ya nchi yetu yatakayotumika kuendesha mashindano ya AFCON mwaka 2019 kwa vijana chini ya umri wa miaka 17, utafanywa na Kamati ya Maandalizi ya Mashindano ya AFCON 2019 iliyotangazwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo siku ya Jumamosi tarehe 11/11/2017 Jijini Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, maandalizi ya mashindano haya ukiwemo uteuzi wa maeneo ya kuendeshea mashindano hayo, ni sehemu ya hadidu za rejea za Kamati hiyo ambayo Mwenyekiti wake ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. Makamu wake ni Mjumbe wa Kamati Tendaji ya Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) ndugu Leodger Tenga na Mtendaji wake mkuu ni Makamu wa Rais wa Kamati ya Olimpiki ya Tanzania, ndugu Henry Tandau.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kazi kubwa inayoikabili Kamati hii ni uboreshaji wa miundombinu kwa viwango vya Kimataifa, kazi ya uteuzi wa maeneo ya kuendeshea mashindano hayo itafanyika mapema iwezekanavyo. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Je, ni lini Wilaya ya Lushoto itaanza tena kupokea matangazo ya Redio ya Taifa (TBC)?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kijiografia Wilaya ya Lushoto katika Mkoa wa Tanga ni kati ya Wilaya ambazo zinazozungukwa na milima, mazingira ambayo huzuia mawimbi ya TBC FM pamoja na TBC Taifa, ambayo hurushwa kutokea mitambo ya FM iliyoko katika eneo la Mnyuzi Wilayani Muheza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua changamoto hii, TBC imeamua sasa mtambo wa kurushia matangazo hayo ujengwe katika Wilaya ya Lushoto ili matangazo ya redio yaweze kufika kwa uhakika katika wilaya hii. Ili kufanikisha kazi hii, TBC imetenga shilingi milioni 50 toka bajeti yake ya ndani kwa ajili ya mnara utakaotumika kuweka mtambo wenye nguvu ya watt 500 na viunganishi vyake kwa ajili ya kupokea matangazo hayo. Mtambo huu utafungwa katika eneo la Kwemashai ambako kuna miundombinu ya kuwezesha zoezi hili kukamika kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-
Wananchi wa Wilaya ya Chunya wameanza kujenga uwanja wa michezo wa kisasa wa Wilaya.
Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia ujenzi huu ili ukamilike haraka?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Victor Kilasile Mwambalaswa, Mbunge wa Lupa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995 kifungu cha 5.1.8(b) (vi) inaelekeza wajibu wa mamlaka ya Serikali za Mitaa kushirikiana na wananchi katika kujenga, kulinda na kutunza miundombinu ya michezo ikiwemo viwanja vya michezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi wa uwanja wa michezo wa Chunya unatekelezwa kwa kuzingatia sera ya michezo ikisimamiwa na Serikali kupitia Halmashauri ya Chunya kwa ushirikiano wa karibu na wananchi pamoja na wadau. Mradi huo unaotarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi bilioni nane umetumia kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 100 zilizotolewa na Hamashauri ya Wilaya ya Chunya katika mwaka huu wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Seriakli kupitia Halmashauri ya Chunya imetenga kiasi cha shilingi milioni 50 kwa ajili ya kuendelea na hatua mbalimbali za mradi wa ujenzi wa uwanja huo wa michezo.
MHE. PROSPER J. MBENA aliuliza:-
Kutokana na kuongezeka kwa matangazo ya biashara kwenye vyombo vya habari, upo uwezekano wa baadhi ya matangazo hayo kuwakera na kuleta hisia tofauti kwa baadhi ya watu na hasa watoto kutokana na maudhui mabaya ya baadhi ya matangazo haya.
(a) Je, Serikali haioni kuna umuhimu wa kuunda chombo cha kusimamia maudhui ya matangazo ya kibiashara ili kuweka na kusimamia taratibu na kanuni za matangazo?
(b) Je, ni idara gani ya Serikali inahusika moja kwa moja na malalamiko ya wananchi dhidi ya kampuni na taasisi zinazotoa matangazo yenye athari kwa jamii?
(c) Je, ni hatua gani zinachukuliwa dhidi ya kampuni hizo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prosper Joseph Mbena, Mbunge wa Morogoro Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tayari ina vyombo vya kusimamia maudhui ya vyombo vya habari nchini, yakiwemo maudhui katika matangazo. Vyombo hivyo ni Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) inayoundwa chini ya kifungu cha Sheria Na. 4 cha Mamlaka ya Mawasiliano Na. 12 ya mwaka 2003, ambayo ina Kamati ya Maudhui iliyoundwa chini ya kifungu cha 26 cha sheria hiyo na marekebisho yake katika kifungu cha 173 cha Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroni na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010. Kamati hii ndiyo inayosimamia maudhui ya matangazo ya kielektroniki (redio, television na mitandao ya kijamii).
Mheshimiwa Naibu Spika, chombo cha pili ni Bodi ya Filamu Tanzania ambayo vilevile inasimamia maudhui katika picha jongevu zinazorushwa katika majumba ya sinema, hadharani vilevile katika michezo ya kuigiza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Idara ya Habari Maelezo ni chombo cha tatu ambacho kimehuishwa chini ya kifungu cha Sheria Na. 4 na Sheria Na. 5 vya Sheria ya Huduma ya Habari Namba 12 ya mwaka 2016 kinachosimamia maudhui katika machapisho mbalimbali yakiwemo magazeti, majarida pamoja na vipeperushi.
Mheshimiwa Naibu Spika, zipo hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali inapobainika bila kutia shaka kuwa kampuni, asasi au taasisi imechapisha ama kutoa tangazo lenye athari kwa jamii. Hatua hizo ni pamoja na kupewa onyo, kufungiwa kutoa huduma kwa kipindi kitakachotajwa au kufungiwa kabisa kutokujihusisha na utangazaji au uchapishaji wa habari pamoja na matangazo. Serikali inaendelea kuhimiza jamii nzima kuendelea kuzingatia sheria na taratibu zilizopo katika kusambaza habari mbalimbali kwa jamii.
MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza:-
Tunatambua kuwa michezo duniani kote imekuwa chanzo cha mapato na kuinua uchumi wa Taifa husika, lakini nchini Tanzania michezo hususan soka imebaki kuwa burudani tu.
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuinua Soka la Tanzania?
(b) Je, kuna mahusiano gani kati ya Serikali na TFF
katika kuimarisha soka la Tanzania kuanzia ngazi ya Wilaya?
(c) Je, Shirikisho la Mpira wa Tanzania (TFF) linapata fedha za ruzuku kiasi gani toka FIFA na Wadhamini kama TBL na Serengeti Breweries?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhan Sima, Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika kuhakikisha kuwa michezo ikiwepo soka inaimarika nchini, imeendelea kuendesha mashindano mbalimbali ya michezo mashuleni kitaifa ikiwepo UMISETA pamoja na UMITASHUMTA ili kuibua vipaji mapema na imeteua shule 56, mbili kwa kila mkoa hadi tatu kwa kila mkoa ili ziwe shule za michezo kwa ajili ya kukuza na kuendeleza vipaji vya michezo ikiwepo mchezo wa soka.
Aidha, Serikali kupitia Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya, imeendelea kutoa mafunzo ya muda mfupi na mafunzo ya muda mrefu kwa wakufunzi wa michezo mbalimbali ukiwepo mchezo wa mpira wa miguu.
b) Mheshimiwa Mwenyekiti, TFF, vyama vya michezo pamoja na mashirikisho mengine ya michezo vimesajiliwa na kufanya kazi chini ya Sheria ya Baraza la Michezo (BMT) Na. 12 ya mwaka 1967 na marekebisho yake ya mwaka 1971. Aidha, TFF inaendelea na uboreshaji wa viwanja vya soka nchini, mfano ni viwanja vya Kaitaba na Nyamagana mkoani Mwanza. Vilevile TFF inatoa msaada wa kiufundi katika viwanja mbalimbali ili kuhakikisha kwamba viwanja vinakuwa katika ubora unaotakiwa. Wizara yangu inaunga mkono programu mbalimbai za TFF katika kukuza mchezo wa mpira wa miguu wilayani na mikoani zikiwemo programu mpya kabisa za grass root pamoja na programu ya live your goals kwa wanawake ambazo zilizinduliwa Mkoani Kigoma Februari, 2018. BMT nayo inaendelea kusimamia utekelezaji wa Katiba, Kanuni na Sheria zinazosimamia michezo mbalimbali nchini.
c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mapato ya TFF; kwanza TFF ina udhamini wa miaka minne (2015-2018) kutoka FIFA kwenye programu ya FIFA Forward ambayo hutoa kiasi cha dola za Kimarekani milioni 1.25 kwa mwaka ambapo kati ya hizo dola za Kimarekani 750,000 hutumika kwa ajili miradi ya maendeleo na dola za Kimarekani 500,000 hutumika kwa ajili ya gharama za kuendeshea ofisi, timu za Taifa pamoja na ligi. Fedha hizi za maendeleo hazikuwahi kutolewa na FIFA tangu mwaka 2015, hivyo, TFF wanatarajia kupokea kiasi fedha cha dola za Kimarekani milioni tatu kwa ajili ya kutekeleza miradi husika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, TFF iliingia mkataba na Kampuni ya Bia ya TBL mwaka 2013-2017 kwa thamani ya Dola za Kimarekani milioni 10 kwa ajili ya Timu ya Taifa ambap kwa sasa mkataba huo umeshamalizika. Hivyo, TFF imeingia mkataba wa ufadhili na Kampuni ya Bia ya Serengeti wa miaka mitatu (2017-2019) wenye thamani ya shilingi milioni 700 kwa ajili ya timu ya Taifa ya wanaume na shilingi milioni 450 kwa ajili ya ligi kuu ya wanawake nchini.
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI (K.n.y. MHE. NURU A. BAFADHILI) aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani madhubuti wa kuhakikisha vijana wetu wanakuwa na maadili pamoja na silka na desturi za Kitanzania kama walivyo wazazi wao?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nuru Awadhi Bafadhili, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nianze kwa kusisitiza kuwa wazazi na familia kwa ujumla ndiyo walezi wa kwanza wenye jukumu la makuzi ya mtoto kuanzia hatua za awali. Wazazi hufuatiwa na vyombo vya elimu kuanzia elimu ya awali, msingi, sekondari hadi elimu ya juu. Jukumu la kusimamia malezi na makuzi ya watoto na vijana ni pamoja na kuelimisha kwa maneno na vitendo kuhusu utambuzi wa mambo mema na mambo mabaya, mambo yanayofaha na mambo yasiyofaha yanayostahili na yasiyostahili yakiwemo masuala ya mavazi, kauli, staha, mwenendo pamoja na muonekano kwa vijana.
Mheshimiwa Spika, hatua ya awali ya malezi ya makuzi ikishapita ndipo wajibu mkubwa wa Serikali unajitokeza katika ukuaji wa vijana kupitia sera, kanuni, sheria, taratibu pamoja na miongozo na kwa kutumia majukwaa mbalimbali ya elimu na nasaha kama vile semina, warsha, makongamano, mikutano, maonesho pamoja na matamasha.
Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa inayolikabili Taifa letu leo ni athari ya utamaduni wa nje kwa maadili, mila na desturi zetu kupitia muingiliano mkubwa wa watu wa dunia kwa njia ya utalii, biashara na kadhalika, vilevile kupitia maendeleo ya kasi ya TEHAMA. Pamoja na juhudi za Serikali kudhibiti wimbi la utamadunisho hasi nchini kwa kutumia sheria, kanuni na vilevile kuboresha mitaala yetu toka shule ya msingi hadi elimu ya juu ili izingatie elimu ya uraia, utaifa, uzalendo, mchango wa wazazi na wananchi kwa ujumla katika kufanikisha jitihada za Serikali hauna mbadala. (Makofi)
MHE. JOSEPH L. HAULE (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:-
Je, Serikali ina mikakati gani ya muda mrefu katika kuimarisha ushiriki wenye tija kwa Tanzania katika mashindano mbalimbali ya kimataifa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako naomba uniruhusu nitumie nafasi hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri kuipongeza timu yetu ya vijana ya Serengeti Boys kwa kuweza kufuzu kuingia mashindano ya nusu fainali katika mashindano ya CECAFA ambayo yanafanyika nchini Burundi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zubeda Hassan Sakuru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na timu zetu za michezo kuonesha kuwa matokeo yasiyoridhisha katika mashindano mbalimbali ya Kimataifa, dalili za Tanzania kurejesha sifa yake ya zamani ya umahiri katika michezo zimeanza kuonekana baada ya mwanariadha wetu nyota Alphonce Simbu kushika nafasi ya tano katika mashindano ya mbio ndefu za Olympic Brazil mwaka 2016. Simbu na wanariadha wengine wa Tanzania waliendeleza rekodi hiyo ya ushindi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Januari 2017, Simbu alinyakua medali ya dhahabu kwenye mashindano ya Kimataifa ya mbio ndefu ya Mumbai – India; Aprili 2017 Cecilia Ginou Kapanga aliipatia Tanzania medali ya dhahabu kwenye mashindano ya Beijing International Marathon nchini China; lakini vilevile tarehe 23 Aprili, 2017 Magdalena Chrispin Shauri alishika nafasi ya tano kati ya wanariadha 25,000 kwenye mashindano ya Hamburg Marathon nchini Ujerumani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Aprili, 2017 Emmanuel Ginouka Gisamoda alikuwa mshindi wa kwanza na kuipatia Tanzania medali ya dhahabu kwenye mashindano ya Shanghai International Half Marathon. Lakini vilevile mwezi Aprili, 2017 Simbu alishika nafasi ya tatu kwenye mashindano makubwa ya London Marathon.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tumeona mafanikio yaliyojitokeza kwenye mchezo wa mpira wa miguu ambapo timu ya Taifa vijana Serengeti Boys ilifuzu kucheza fainali za michuano ya kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 nchini Gabon na kufuta historia hasi tuliyokuwa nayo ya timu zetu kushindwa kufika ngazi hiyo kwa miaka yote 37.
Mheshimiwa Mwenyekiti, somo kubwa tunalojifunza ni umuhimu wa mazoezi toka umri mdogo hivyo mkakati wa Serikali wa muda mrefu ni kama ifuatavyo:-
(i) Kuimarisha michezo shuleni ili kuibua na kulea vipaji vinavyojitokeza. Hivyo basi, shule 56 za sekondari zilizoteuliwa mwaka 2013 na mwaka 2014 na Serikali kila mkoa kuwa shule za michezo hazina budi kuimarishwa kwa vifaa, ufundishaji na miundombinu ili ziweze kutekeleza wajibu wake.
(ii) Katika kuimarisha uongozi katika vyama vya mashirikisho ya michezo mbalimbali nchini kwa kuvisimamia kwa karibu ili vizingatie katiba na sheria za michezo.
(iii) Kuimarisha mashindano ya UMITASHUMTA na UMISETA ambayo ndiyo kisima kikubwa cha kuwapata wanamichezo wa michezo yote nchini. Ahsante. (Makofi)
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-
Tanzania inayo makabila yapatayo 124 yanaongea lugha tofauti na yanazo mila tofauti ambazo wamekuwa wakiziheshimu tangu enzi za mababu:-
(a) Je, ni lini Serikali itaandika lugha za makabila hayo ili yasiweze kupotea kwenye uso wa dunia?
(b) Je, ni lini Serikali itaandika historia kwa kila kabila nchini ili vijana wanaokua waweze kujua tamaduni za makabila yao?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, lenye vipengele (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali ni msimamizi na mratibu wa shughuli mbalimbali za utamaduni nchini. Aidha, kwa mujibu wa Sera ya Utamaduni ya mwaka 1997, jamii ndiyo mmiliki wa utamaduni, hivyo wajibu wa kufanya tafiti, kuorodhesha na kuandika historia za kila jamii ni wetu sote.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa upande wake inaendelea na utaratibu wa kukusanya tafiti za lugha za jamii mbalimbali zinazofanywa na wadau wanaojishughulisha na ustawi wa lugha nchini na inaandaa kanzidata ili lugha hizo zisipotee kwenye uso wa dunia. Hadi sasa lugha za jamii 38 zimeshakusanywa na kufanyiwa tafiti na zimehifadhiwa kwa njia ya kamusi. Ikumbukwe kuwa lugha ni sehemu ya utamaduni wa Taifa lolote lile.
Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali na wadau mbalimbali wameandika na wataendelea kuandika historia za jamii, mila na desturi zake. Kwa sasa, karibu kila jamii imekwishaandika historia ya mila na desturi zake. Wizara inaendelea na utaratibu wa kukusanya maeneo ya kihistoria ya jamii mbalimbali hapa nchini na kuyahifadhi kwa njia ya TEHAMA. Vitabu vya historia na maandiko hayo yanapatikana katika Ofisi za Idara ya Nyaraka za Taifa, maktaba pamoja na maduka mbalimbali ya vitabu nchini.
MHE. MARTHA M. MLATA (K.n.y. MHE. AISHAROSE N. MATEMBE) aliuliza:-
Sanaa ya Maigizo na muziki ni miongoni mwa Sekta zinazochangia asilimia kubwa ya vijana kujiajiri lakini kuna Vyuo vichache nchini vinavyotoa elimu hiyo ya sanaa ya muziki na maigizo ambavyo ni Chuo cha Sanaa Bagamoyo na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam huku masharti yake yakiwa ni changamoto kwa vijana wa mikoani:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha matawi ya Vyuo hivyo kwenye Kanda ama Mikoa ili kuongeza fursa zaidi kwa vijana?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Aisharose Ndogholi Matembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mafunzo ya Elimu ya Sanaa ya Maigizo na Muziki au kwa ujumla Sanaa, yanatolewa kwa ngazi ya Shahada na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Dodoma na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam kwa upande wa Serikali na Chuo Kikuu cha Tumaini Arusha kwa upande sekta binafsi. Aidha, mafunzo kwa ngazi ya Stashahada na Cheti kwa Vyuo vya Serikali hutolewa na Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) yenye matawi takribani nchi nzima. Vipo vilevile vyuo binafsi ambavyo hutoa mafunzo ngazi ya Stashahada pamoja na Cheti.
Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa vijana na wadau wengine wanaotaka kubobea kwenye sanaa wajiunge na vyuo hivi ambavyo vimetawanyika nchi nzima. Aidha, nawapongeza wadau wote walioanzisha vyuo hivyo ili kuunga mkono jitihada za Serikali.
MHE. VEDASTO EDGA NGOMBALE (KILWA KASKAZINI)
aliuliza:-
Kupata habari ni moja ya haki za Kiraia, TBC ni chombo pekee cha habari kwa sasa kinachowafikia wananchi wengi hususan wale wanaoishi vijijini lakini kwa muda mrefu sasa chombo hicho hakisikiki vizuri katika maeneo mengi ya vijijini vya Jimbo la Kilwa Kaskazini na Wilaya ya Kilwa kwa ujumla.
Je, ni tatizo gani linalosababisha chombo hiki kisisikike vizuri katika maeneo mengi ya vijijini?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto Edga Ngombale, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshaanza kuchukua hatua mahsusi za kuboresha usikivu wa Redio katika Mikoa ya Lindi pamoja na Mtwara, ikiwemo Wilaya ya Kilwa kama ifuatavyo:-
(a) Mitambo ya kurushia matangazo iliyoko Nachingwea ya TBC Taifa imeongezewa nguvu kutoka watt 250 hadi watt 1,000 na ile ya TBC FM toka watt 150 hadi watt 1,000. Matokeo yake ni usikivu bora wa redio maeneo mengi ya Nachingwea, Ruangwa na sehemu za Wilaya ya Masasi.
(b) Mitambo miwili ya kurushia matangazo ya TBC Taifa na TBC FM imejengwa Mtwara, kila mmoja una ukubwa wa watt 1,000 na kuwezesha matangazo ya redio kuwafikia wananchi Mtwara Vijijini, Tandahimba pamoja na Lindi Vijijini.
(c) Hatua ya tatu ni ndani ya mwaka wa fedha 2018/2019 tuna mradi wa kujenga Mtambo mpya wa FM wa kurusha matangazo eneo la Nangurukuru ambao utaimarisha usikivu wa redio maeneo ya milima yaliyobaki.
MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-

FIFA inatoa misaada ya fedha kwa Tanzania kupitia TFF:-

Je, ni kiasi gani cha fedha TFF imekuwa ikiipatia Zanzibar kupitia ZFA?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli FIFA inatoa msaada wa fedha kwa mashirikisho ya mpira wa miguu ikiwepo TFF kwa ajili ya miradi na programu mbalimbali. Fedha hizo huwa ni maelekezo maalum kwa lengo la kusaidia na kuendeleza maeneo mahususi yafuatayo: Ligi ya Wanawake, ligi ya vijana, masuala ya kiutawala, kuinua vipaji kwa (Grassroot Program), Women’s Football Promotion, pamoja na Maendeleo ya Waamuzi.

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwaka huu FIFA itakuwa inatoa jumla ya Dola za Kimarekani milioni 1.25 kila mwaka kwa wanachama wake wote ikiwepo ZFA, ambayo ni sehemu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania kwa mchanganuo ufuatao: fedha za miradi ya maendeleo kiasi cha Dola za Kimarekani 750,000, fedha kwa ajili ya kuendesha ofisi, Dola za Kimarekani 500,000.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kwa muda wa miaka mitatu sasa kutokana na kutokuwepo kwa uwazi katika matumizi ya fedha na kutokidhi vigezo vya utawala bora, TFF wamekuwa hawapati fedha hizo. Kazi kubwa imeshafanyika kurekebisha dosari zilizokuwepo za kiuhasibu na kiutawala bora. Hivyo, uwezekano ni mkubwa kwa TFF na ZFA kupokea fedha za msaada huo wa fedha mapema mwaka huu.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. SABREENA H. SUNGURA) aliuliza:-

Michezo ni afya, furaha, burudani, undugu na pia huondoa au kupunguza uhalifu nchini. Kuwa na viwanja vyenye hadhi kama kile cha Jakaya Kikwete Youth Park huvutia vijana wengi nchini kupenda michezo:-

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga viwanja vyenye hadhi hiyo nchi nzima?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sabreena Sungura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ujenzi wa viwanja vya michezo nchini si suala la Serikali peke yake bali jamii nzima ya Watanzania zikiwemo taasisi za umma, asasi za kiraia na kampuni za watu binafsi. Wajibu wa Serikali ni kuonesha njia kwa ujenzi mkubwa wa viwanja changamani kama vile Uwanja wa Taifa na Uwanja wa Uhuru ulioko Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, viwanja vyote viwili sasa hivi viko katika ukarabati mkubwa utakaogharimu zaidi ya shilingi bilioni tatu ili kujiweka tayari kwa Mashindano ya Mpira wa Miguu wa Bara la Afrika kwa watoto chini ya umri wa miaka 17 yatakayofanyika mwezi wa Nne mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na ukarabati huo mkubwa Serikali imekamilisha maandalizi yote ya awali na ya kiufundi ikiwemo upatikanaji wa eneo la hati miliki, uwekaji wa mipaka ya eneo lote pamoja na beacons, ununuzi wa gari mbili za mradi huo, tathmini ya kimazingira, tafiti za eneo, upembuzi yakinifu wa mradi na michoro ya ubunifu wa ujenzi wa uwanja huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kiwanja cha Jakaya Mrisho Kikwete Youth Park cha Dar es Salaam anachokiongelea Mheshimiwa Mbunge kimejengwa kutokana na mahusiano ya karibu kati ya Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Ilala chini ya Mbunge wake Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu na Kampuni ya Symbion kwa kushirikiana na Club ya Sanderland.

MWENYEKITI: Hampigi makofi? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo kama ni kuonesha njia Serikali imeshafanyika hivyo na itaendelea kujenga viwanja vingine kadiri mahitaji yatakavyojitokeza na uwezo wa kifedha utakavyopatikana.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kulipongeza Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF) kwa uboreshaji wa Viwanja vya Kaitaba Kagera, Nyamagana Mwanza, na Mikoa ya Iringa, Singida na Lindi kwa kuonyesha njia katika upatikanaji wa viwanja bora vya michezo nchini.
MHE. ESTER A. MAHAWE aliuliza:-

Mkoa wa Manyara, hususani Wilaya ya Mbulu, umewahi kutoa wanariadha mahiri ambao walililetea Taifa heshima kubwa, lakini cha kushangaza wanariadha hao wametelekezwa:-

(a) Je, ni lini Serikali sasa itaandaa utaratibu wa kuwaenzi wanariadha hao?

(b) Je, ni lini sasa Serikali itajenga uwanja kwa ajili ya riadha katika Mkoa wa Manyara ili kuwahamasisha wanariadha wapya?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ester Alexander Mahawe, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, picha anayoichora Mheshimiwa Mbunge ya wanamichezo kutothaminiwa haiendani na hali halisi upande wa wanamichezo nchini waliofanya vizuri na kujituma ipasavyo. Naomba nitoe mifano kadhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanariadha Filbert Bayi aliyevunja rekodi ya dunia ya mbio za mita 1,500 huko New Zealand mwaka 1974 ni Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki ya Tanzania na mmiliki wa Shule za Filbert Bayi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Suleiman Nyambui, mshindi wa medali ya shaba Mashindano ya All African Games mwaka 1978 na medali ya fedha ya Michezo ya Olimpiki 1980 kwa mbio za mita 5,000 sasa ni Kocha wa Riadha wa Taifa wa Brunei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Juma Ikangaa, mshindi wa kwanza wa mbio ndefu za marathon Jijini New York mwaka 1988 na mshindi wa pili mara tatu mfululizo wa marathon Jijini Boston mwaka 1988 – 1990 ni Mjumbe wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na mratibu wa mashindano ya riadha kwa wanawake (ladies first) yanayodhaminiwa na Shirika la Kimataifa la Ushirikiano la Japan (JICA) pamoja na Wizara yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Samson Ramadhani, mshindi wa marathon medali ya dhahabu Australia mwaka 2006 ni Afisa wa Jeshi;

Mheshimiwa Mwenyekiti, Gidamis Shahanga, mshindi wa medali ya dhahabu mbio za marathon nchini Canada mwaka 1978, Uholanzi 1984, Nairobi 1988 na Vienna, Austria 1990 ni Mwenyekiti Mstaafu wa Halmashauri ya Katesh Manyara; na wengine wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanamichezo, wakiwepo wanariadha walioliletea Taifa hili sifa na heshima kubwa wanatoka sehemu mbalimbali za Tanzania. Wizara imeanza mchakato wa kuanzisha makumbusho maalum Uwanja wa Taifa ambapo picha za wanamichezo wote walioliletea Taifa letu heshima katika vipindi mbalimbali zitawekwa.
MHE. FELISTER A. BURA (K.n.y. MHE. LIVINGSTON J. LUSINDE) aliuliza:-

Kwa kuwa Serikali imehamia Dodoma, je, kwa nini Serikali isijenge Maktaba yenye kumbukumbu za kazi za Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambayo pia itakuwa sehemu ya utalii kwa watu wa ndani na nje ya Mkoa wa Dodoma?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, napenda kjibu swali na Mheshimiwa Livingstone Lusinde, Mbunge wa Mtera, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kuzingatia umuhimu wa kuhifadhi kumbukumbu za Waasisi wa Taifa ambao ni Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Abeid Aman Karume, ilitunga Sheria ya Kuwaenzi Waasisi ya mwaka 2004. Sheria hii inaelekeza uhifadhi wa kumbukumbu hizo na kuanzishwa kwa kituo cha kutunza kumbukumbu. Aidha, Umoja wa Afrika uliiteua Tanzania mwaka 2011 kuwa Mratibu wa Programu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika ambayo, pamoja na mambo mengine, imetoa kipaumbele katika uhifadhi wa kazi ambazo alifanya Baba wa Taifa na mashujaa wenzake katika ukombozi wa Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni katika msingi huo Serikali kwa kushirikiana na UNESCO, imekarabati studio za iliyokuwa Redio Tanzania Dar es Salaam zilizopo barabara ya Nyerere na kuwa kituo adhimu cha kuhifadhi na rejea ya kazi za Baba wa Taifa. Serikali vilevile, inaunga mkono juhudi za taasisi kadhaa nchini katika kuhifadhi amali za urithi wa kumbukumbu za Baba wa Taifa. Baadhi ya taasisi hizo ni kama ifutavyo:-

Maktaba ya Taifa, Dar es Salaam; Makumbusho ya Taifa, Dar es Salaam; Makumbusho ya Mwalimu Nyerere, Butiama; Ofisi ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa; Taasisi ya Mwalimu Nyerere; na Vituo vya Television vya TBC na ITV.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa Programu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika, Serikali imeteua Wilaya ya Kongwa, Dodoma kuwa Kituo Kikuu cha Kumbukumbu za Ukombozi wa Nchi yetu ambapo miundombinu kadhaa ya uhifadhi wa historia itajengwa zikiwemo kazi adhimu za Baba wa Taifa. Ahsante.
MHE. MAULID S. A. MTULIA aliuliza:-

Vijana wetu wanafanya kazi za sanaa nzuri sana lakini kipato wanachokipata hakilingani na ubora wa kazi zao:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia vijana hawa kupata stahiki ya kazi zao?

(b) Je, sera na sheria zinasaidiaje wasanii wetu kumiliki na kunufaika na kazi zao za sanaa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maulid Said Mtulia, Mbunge wa Kinondoni, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Utamaduni ya Mwaka 1997 inaelekeza kuanzishwa kwa chombo cha kusimamia hakimiliki ambayo ni sehemu muhimu ya dhana pana ya haki bunifu (intellectual property). Hivyo, mwaka 1999 ikatungwa Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki ambayo chini yake maslahi ya watunzi wa kazi za Sanaa, watafsiri, watayarishaji wa kuhifadhi sauti, wachapishaji na kadhalika yanalindwa kisheria na chombo cha kusimamia haki hizo, yaani Chombo cha Hakishiriki Tanzania (COSOTA).
MHE. MGENI JADI KADIKA aliuliza:-

Utandawazi umechangia sana vijana kupoteza maadili:-

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kwa vijana wetu kuwekewa umri maalum wa kutumia mitandao ili kupunguza mmomonyoko wa maadili?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli utandawazi umechangia sana katika kuleta mmomonyoko wa maadili kwa kiasi kikubwa kwa jamii zetu hususan vijana kupitia intanenti, mitandao ya kijamii na maudhui ya nje kupitia muziki na filamu. Ndiyo sababu ya Serikali kuja na Sheria ya Makosa ya Mtandao (Cybercrime) ya mwaka 2015 na Kanuni za Maudhui ya Mtandao na Maudhui ya Redio na Runinga za mwaka 2018 ambazo zimepigiwa sana kelele ndani ya Bunge hili Tukufu kuwa zinaua uhuru.

Mheshimiwa Spika, wazazi na familia kwa ujumla ndio walezi wa kwanza wenye jukumu la kumlea mtoto kuanzia hatua ya awali na hufuatiwa na Taasisi za elimu ya awali, msingi, sekondari hadi elimu ya juu ambao huwaelimisha kwa maneno na vitendo watoto na vijana hususan utambuzi wa mambo mema na mabaya, yanayofaa na yasiyofaa. Baada ya hatua hizi kupita ndipo wajibu mkubwa wa Serikali unajitokeza.
MHE. MAULID S. MTULIA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuimarisha Sekta ya Michezo kwa kuandaa Wakufunzi wa Michezo, kujenga viwanja vya kisasa na kuhakikisha upatikanaji wa vifaa vya michezo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maulid Said Mtulia, Mbunge wa Kinondoni, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha Sekta ya Michezo, Serikali imeendelea kutoa mafunzo ya aina mbalimbali yanayohusu taaluma tofauti za Michezo. Kupitia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, elimu ya michezo hutolewa katika ngazi ya Shahada kupitia idara ya maalum ya Physical Education and Sports Science. Aidha, kupitia Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya, Mkoani Mwanza, Serikali inaendelea kutoa mafunzo ya utawala katika Michezo pamoja na ukufunzi katika michezo mbalimbali katika ngazi ya Stashahada, Diploma in Sport Admistration and Coaching ambayo hutolewa kwa muda wa miaka miwili.

Mheshimiwa Spika, suala la ujenzi wa miundombinu siyo la Wizara peke yake, letu sote ikiwemo sekta binafsi na halmashauri zote nchini.
MHE. NASSOR SULEIMAN OMAR aliuliza:-

Utamaduni katika kila nchi ni utambulisho wa Taifa; na kwa kuwa kuna upotevu mkubwa wa utamaduni wa asili kwenye makabila yetu nchini:-

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kufufua utamaduni wa asili wa makabila yetu?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nassor Suleiman Omar Mbunge wa Ziwani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Serikali ni msimamizi na mratibu wa shughuli zote za utamaduni ikiwepo sera ya utamaduni na sheria zinazohusu utamaduni jamii ndio mmiliki wa utamaduni. Hivyo, nitumie fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge akiwemo muuliza swali, taasisi, asasi na mashirika ya jamii nzima ya watanzania kuwa mstari wa mbele katika kulinda utamaduni wetu na kufufua pale unapofifia. Wizara yangu inatambua na kupongeza mwamko mpya katika jamii wa kuhimiza na kuendeleza utamaduni wetu maeneo kadhaa nchini kwa mfano: Tamasha la ngoma ya utamaduni la Dkt. Tulia Traditional dance ambalo linafanyika katika Mkoa wa Mbeya. Tamasha la majimaji Serebuka Songea, Tamasha la Bulambo ambalo linafanyika Mwanza, Tamasha la Chamwino Dodoma, Tamasha la Nyasa na Matamasha ya makabila mbalimbali yanayoendelea katika Kijiji cha Makumbusho Jijini Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Serikali wizara yangu mbali na kuhimiza matumizi ya lugha ya Kiswahili ndani na nje ya nchi inaendelea na tafiti za kiutamaduni za makabila mbalimbali nchini lengo likiwa ni kuhifadhi. Mkazo zaidi umewekwa kwenye tamaduni za makabila au jamii zenye wazungumzaji wachache ambao zipo katika hatari ya kutoweka. Aidha, wizara inashirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii katika kuendesha tamasha jipya la urithi wa utamaduni inasimamia kila mwaka tamasha la kimataifa ya sanaa na utamaduni Bagamoyo ambao ni kivutio kikubwa kwa wanasanaa, wadau wa sanaa na wapenzi wa sanaa kutoka ndani na nje ya nchi na kwa sasa wizara inaratibu tamasha la utamaduni wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (JAMAFEST) litarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 21 hadi 28 mwezi mwaka na mwaka huu na kuwavutia wanasanaa na wadau takribani laki moja kutoka ndani na nje ya Jumuiya.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA aliuliza:-

Baadhi ya mechi za mpira wa miguu za Ligi Kuu Tanzania Bara 2018/2019 zilichezwa bila kuwepo kwa gari la wagonjwa uwanjani na kusababisha wachezaji walioumia kulazimika kukimbizwa Hospitali kwa kutumia magari ya kawaida:-

(a) Je, Serikali ina taarifa juu ya tatizo hilo?

(b) Je, Serikali ina mkakati gani katika kuhakikisha kosa hilo halitokei tena viwanjani?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Ally Mtolea, Mbunge wa Temeke, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu na sharti la kuwepo kwa magari ya wagonjwa viwanjani ili kuhudumia wachezaji na hata watazamaji wanaopatwa na dharura kubwa za kiafya na dharura inayohitaji huduma haraka ya matibabu. Aidha, Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF) linaheshimu Kanuni hiyo pamoja na kwamba utekelezaji wake katika baadhi ya mechi za Ligi Kuu unakawamishwa na uhaba wa magari ya wagonjwa ambayo huchelewa kufika uwanjani siyo kwa makusudi bali ni kwa kutingwa na huduma zingine za tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, ni mechi ya Mbao FC dhidi ya Coastal Union iliyochezwa katika Uwanja wa CCM-Kirumba ambapo mchezaji aliumia kipindi cha kwanza lakini gari la kubebea wagonjwa lilikuja kipindi cha pili kutokana na gari hilo kuwa na majukumu mengine Mkoani hapo. Hali hii inasababishwa na ukweli kwamba hakuna Chama cha Soka cha Mkoa kinachomiliki magari ya wagonjwa, magari yote yanapatikana kwenye Halmashauri husika, baadhi ya hospitali za Serikali na asasi zenye magari ya wagonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, natoa wito kwa Kamati za Michezo za Mikoa na Wilaya kushirikiana kwa karibu na mamlaka nilizozitaja kwenye huduma hii ili kuepusha madhara makubwa yanayoweza kutokea kwa kukosa huduma hiyo inapohitajika. Aidha, nawahimiza TFF na uongozi wake wa Mikoa kujiongeza kwa kufikiria njia rahisi zaidi za kubebea majeruhi kama vile pikipiki maalum za miguu mitatu au miwili kwenye mechi za ligi ya chini ili kuepusha madhara makubwa yanayoweza kutokea kwa majeruhi kucheleweshwa kupelekwa hospitalini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-

Michezo mingi ikiwemo mpira wa miguu inapata ufadhili sana hapa nchini kupitia kampuni mbalimbali binafsi na za Kiserikali:-

Je, ni lini Serikali itahakikisha ufadhili unapatikana kwenye michezo inayohusu wanawake hususan michezo ya ngumi kwa wanawake?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nisahihishe dhana ya kwamba michezo inayowahusisha wanaume inapata “ufadhili sana” nikinukuu maneno aliyotumia Mheshimiwa Mbunge, kuliko inayowahusisha wanawake. Mfano hai ni Ligi Kuu ya Mpira wa Miguu upande wa Wanaume kwa msimu wa 2018/2019 ambayo ilikosa udhamini na kusababisha matatizo makubwa ya maandalizi na usafiri kwa timu zote 20 zilizoshiriki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ufadhili haushinikizwi na Serikali bali ni suala la hiari upande wa wafadhili ambao huchukua hatua hiyo wakishaziona fursa za kibiashara na kijamii upande wao. Wajibu wa Serikali ni kujenga mazingira rafiki ya ufadhili huo bila kujali jinsia. Hivi sasa Tanzania ina Ligi Kuu ya Mpira wa Miguu kwa Wanawake ambayo inadhaminiwa na Kampuni ya Vinywaji ya Serengeti Breweries kupitia bia yake ya Serengeti Lite.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa riadha, Kampuni ya Multichoice imekuwa mstari wa mbele kudhamini wanariadha bora wanaojitokeza na kuandaa makambi ya mazoezi bila ubaguzi wa jinsia. Kampuni ya SportPesa pekee imejitokeza kumfadhili Mwanamasumbwi Mwakinyo aliyekuwa namba 174 kwa ubora Duniani katika uzito wake, baada ya kumtwanga Eggington wa Uingereza, wakati huo namba akiwa 8 kwa ubora duniani. Hakuna kigezo kingine kilichotumika na SportPesa kumfadhili Mwakinyo zaidi ya weledi aliouonesha katika mchezo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuwaomba wadau wote wa michezo nchini wakiwemo Waheshimiwa Wabunge, kusaidia kushawishi makampuni, taasisi na wadau wenye uwezo kifedha, kudhamini na kufadhili maendeleo ya michezo yote nchini ukiwemo mchezo wa ndondi upande wa wanawake.
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-

TBC ni Shirika la Umma na hutangaza habari na vipindi mbalimbali ili Watanzania wasikie kwa Lugha ya Kiswahili; Tanzania pia ina wageni kutoka nchi mbalimbali duniani waishio nchini. Lakini TBC limekuwa likitangaza taarifa za habari na vipindi vyake vingine kwa lugha ya Kiswahili tu; zamani kulikuwa na kipindi cha External Service kilichokuwa kikitangazwa kwa Lugha ya Kiingereza ili wageni waishio nchini wasikie lakini sasa hivi hakipo.

(a) Je, ni kwa nini TBC ilifuta kipindi cha External Service kilichokuwa kikitangaza taarifa ya habari kwa Lugha ya Kiingereza?

(b) Je, kwa kutangaza taarifa ya habari kwa Kiswahili tu hatuoni kwamba tunawanyima wageni fursa ya kujua kinachoendelea nchini?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwani niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Taska Restituta Mbogo Mbunge wa Viti Maalum lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Idhaa ya External Service ya Radio Tanzania Dar Es Salaam ilianzishwa rasmi wakati wa harakati za kupigania uhuru katika nchi za kusini mwa Afrika ikiwepo, Msumbiji, Zimbabwe, Namibia, Angola, Afrika ya Kusini. Viongozi wa wapigania uhuru katika nchi hizo waliishi na kuratibu harakati za ukombozi kutokea Tanzania ambapo walirusha ya Radio ya kuhamasisha wananchi wao kushiriki katika mapambano hayo kupitia Idhaa hiyo ya External Service. Baada ya nchi hizo kupata uhuru, Idhaa hiyo haikuendelea tena na hayo matangazo yake.

(b) Hata hivyo, kwa sasa TBC kupitia stesheni yake ya TBC International inayopatikana katika masafa ya 95.3, hutangaza kwa lugha ya Kiingereza. Aidha, TBC1 pamoja na TBC Taifa zinarusha baadhi ya vipindi kwa Kiingereza. Kwa mfano TBC1 ina vipindi maarufu “This Week in Perspective” na “International Sphere” na TBC Taifa ina vipindi ya”Breakfast Express”, “Daily Edition”, “Day Time” Overdrive kwa Kiingereza. Vipindi hivi huzungumzia masuala mbalimbali yakiwepo ya kisiasa, kiuchumi, pamoja na kijamii.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kwa kutangaza taarifa ya habari kwa lugha moja ya Kiswahili kunawanyima wageni fursa ya kujua masuala mbalimbali yanayoendelea hapa nchini. Lakini yapo magazeti mbalimbali yanayochapisha habari hizo zinazotokea nchini kwa lugha ya Kiingereza. Magazeti hayo ni pamoja na Daily News, The Guardian, The Citizen.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-

(a) Je, ni sababu zipi zinazosababisha matangazo ya Shirika la Habari Tanzania (TBC) hasa upande wa Radio yasisikike kwenye Tarafa za Kitunda na maeneo mengi ndani ya Jimbo la Sikonge?

(b) Je, ni lini Serikali itarekebisha tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako kwanza naomba nitumie fursa hii kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuipongeza Timu yetu ya Taifa, Taifa Stars, kwa kutuheshimisha sisi kama Taifa kwa kuitoa Timu ya Burundi kwa mikwaju ya penati na hatimaye kuweza kutinga kwenye hatua ya makundi.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijielekeze kwenye swali; kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, TBC kwa Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2016/2017 ilitekeleza mradi wa upanuzi wa usikivu katika wilaya tano zilizopo mipakani mwa nchi yetu; wilaya hizo ni pamoja na Wilaya ya Longido Mkoani Arusha, Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro, Wilaya ya Tarime Mkoani Mara, Wilaya ya Nyasa Mkoani Ruvuma na Wilaya ya Kibondo Mkoani Kigoma. Aidha, Bajeti ya Mwaka 2017/2018 TBC ilitekeleza mradi wa upanuzi wa usikivu katika Mkoa wa Mtwara na Wilaya ya Lushoto Mkoani Tanga. Hadi kufikia tarehe 04 Mei, 2019 shirika lina vituo 33 vya kurushia matangazo katika masafa ya FM kwenye wilaya 102.

Mheshimiwa Spika, TBC inaendelea na mpango wa kupanua usikivu maeneo yote ya nchi nzima, kutegemeana na upatikanaji wa fedha ili kukamilisha wilaya zote 59 ikiwepo Wilaya ya Sikonge. Aidha, TBC ina mpango wa kufanya maboresho katika mitambo yake iliyopo Tabora Kaze Hill kisha kufanya tathmini ya usikivu na kubainisha maeneo yanayopaswa kufungiwa mitambo mingine ili kuleta usikivu Mkoa mzima wa Tabora ikiwepo Wilaya ya Sikonge.

Mheshimiwa Spika, katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2019/2020, TBC inaendelea kutekeleza mradi wa upanuzi wa usikivu katika maeneo ya Mikoa ya Unguja, Pemba, Simiyu, Njombe, Songwe pamoja na Lindi. Mkakati wa Serikali ni kuiwezesha TBC kufikia usikivu katika maeneo yote ya Tanzania.
MHE. GRACE V. TENDEGA (K.n.y. MHE. DEVOTHA M. MINJA) aliuliza:-

Timu ya Taifa ya Wanawake Twiga Stars imefanya vizuri na kuliletea Taifa heshima miaka iliyopita hivi karibuni:-

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhamasisha soka kwa wanawake katika ngazi za wilaya na mikoa kuwa na timu za soka za wanawake kama ilivyo kwa wanaume?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Timu ya Soka ya Taifa ya Mwanawake (Twiga Stras) pamoja na ile ya Kilimanjaro Queens miaka ya hivi karibuni zimefanya vizuri na kuliletea taifa heshima. Kwa kutambua mchango wa wanawake katika kukuza soka la nchi yetu Serikali kwa kushirikiana na wadau hususani Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini Tanzania, imejipanga kutekeleza yafuatayo:-

(i) Serikali inaendelea kusajili vyama na vilabu mbalimbali vya michezo pamoja na kutoa wito kwa wananchi kuendelea kusajili vilabu vyao vikiwemo vya soka la wanawake;

(ii) Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wananchi wote kushiriki katika michezo ukiwemo mpira wa miguu kwa wanawake;

(iii) Serikali kupitia Baraza la Michezo la Taifa (BMT) limeendelea kujenga mazingira mazuri kwa vyama na mashirikisho ya michezo kufaya kazi zao. Baraza la Michezo la Taifa (BMT) pia wameridhia kuanzishwa kwa ligi ya wanawake ya mpira wa miguu;

(iv) Mafunzo mbalimbali ya ukocha na uamuzi wa mpira wa miguu kwa wanawake yametolewa na kwamba tunao wanawake waamuzi (referees) wanaotambulika na Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuwahamasisha wanawake kujihusisha katika kucheza mpira wa miguu kwa kuwa ni mchezo maarufu na kwamba utatoa fursa ya ajira kwa mtoto wa kike.
MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS aliuliza:-

Upimaji wa Afya za Wanamichezo ni jambo muhimu kwa ajili ya kulinda na kuhakikisha afya zao kabla ya kushiriki michezoni kwani kumekuwa na matokeo mbalimbali ya Wanamichezo kupoteza maisha wakiwa uwanjani. Mathalani, Ismael Mirisho wa Timu ya Mbao FC, Marc Vivien Foe wa Cameroon na Cheikh Tiote wa Ivory Coast:-

Je, Serikali kupitia Vyama vya Michezo vimeweka utaratibu gani kuhakikisha upimaji wa afya za wanamichezo ni jambo linalopewa kipaumbele?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri, wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Haji Khamis, Mbunge wa Nungwi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia na kuwa na uelewa sahihi kuhusu umuhimu wa afya za wachezaji wetu wakiwa michezoni. Matukio ya wanamichezo kupata matatizo ya kiafya na hata wakati mwingine vifo kutokea uwanjani, yamekuwa yakitokea mara kwa mara Tanzania na imeshuhudiwa matukio kama hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia ukweli huo, Wizara yangu kupitia kitengo chake cha Kinga na Tiba kwa kushirikiana na Chama cha Madaktari wa Michezo Nchini, imeendelea kutoa elimu ya afya kwa wanamichezo na Viongozi wa Mashirikisho ya Vyama vya Michezo kwa lengo la kuwawezesha kuelewa umuhimu wa huduma za afya kwa wanamichezo muda wote wawapo viwanjani kwa mazoezini au katika mashindano.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo huo, vilabu vyote vya soka vya ligi kuu ya Tanzania kwa mfano, vimeelekezwa kuwa na Daktari mwenye sifa na ambaye muda wote atakuwa tayari kutoa huduma ya matibabu kwa wachezaji.

Mheshimiwa Spika, Kitengo cha Kinga na Tiba cha Wizara, mbali ya kutoa elimu ya afya kwa wanamichezo pia kina jukumu la upimaji wa afya na kutoa Huduma ya Kwanza kwa wanamichezo kila wanaposhiriki michezo au mashindano mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, suala la huduma za afya kwa wanamichezo ni suala la kisera. Sera ya Maendeleo ya Michezo ya Mwaka 1995 sehemu ya 10.1 imeelekeza kuwa ni lazima mchezaji achunguzwe afya yake na kuwekewa kumbukumbu zote za kiafya kwa kipindi chote awapo kambini na ahudumiwe na Daktari kwenye taaluma ya tiba kwa wanamichezo.

Aidha, utaratibu wa matibabu kwa wanamichezo ujumuishe mafunzo juu ya athari za kutumia madawa ya kuongeza nguvu kwa wanamichezo. Wizara yangu inashauri na kuelekeza Vyama na Mashirikisho yote ya Michezo Nchini kuwa na utaratibu wa mara kwa mara wa kutoa elimu ya afya kwa wadau wake pamoja na kutoa elimu kinga kwa wanamichezo ili kulinda afya zao. Wizara yangu iko tayari kutoa ushirikiano katika jitihada hizo kwa kutoa ushauri wa kitaalamu ili kuimarisha afya za wanamichezo.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD aliuliza:-

Ni muda mrefu Serikali ilikuwepo kwenye mchakato wa kupata Vazi la Taifa.

(a) Je, Serikali imefikia hatua gani ya mchakato huo?

(b) Je, ni lini Watanzania wategemee kuwa na Vazi la Taifa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Kombo Hamad, Mbunge wa Wingwi lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato wa Vazi la Taifa ulianza mwaka 2003/2004 na kufufuliwa tena mwaka 2011 baada ya kuona mitindo iliyopatikana haikukidhi haadhi ya kuwa na Vazi la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2011 Kamati ya Kukamilisha Mchakato wa Kupata Vazi la Taifa iliteuliwa ambapo upatikanaji wa Vazi la Taifa ulipitia jatika hatua kadhaa ambazo Wizara ilishirikisha wabunifu na wanamitindo kwa lengo la kushirikisha wadau wa fani hizo ili kupata Vazi la Taifa litakalotambulisha Taifa letu.

Baada ya kamati kumalizia kazi yake ilikabidhi Wizarani taarifa na mapendekezo kuwa Vazi la Taifa litokane na aina ya kitambaa na siyo mshono.Aidha, aina ya vitambaa kwa vazi hilo ilipendekezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Baraza la Mawaziri iliagiza kwamba jamii iachiwe huru kuchagua aina ya vazi ambalo litatokana na mageuzi ndani ya jamii yenyewe na isiwe uamuzi wa Serikali. Wizara ilitoa taarifa kwa maamuzi yaliyofikiwa na Serikali kwenye vyombo vya habari na tovuti ya Wizara ili wananchi wajadili na waamue wenyewe kuhusu Vazi la Taifa ambalo litapendekezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya changamoto zilizojitokezakwa kipindi hicho ni uhamasishaji hafifu wa uvaaji wa Vazi la Taifa. Aidha walitarajia kupokea vazi na siyo kuoneshwa kitambaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya agizo la Waziri Mkuu la kuandaa Tamasha la kupata sura ya Vazi la Taifa ifikapo 30 Desemba, 2018, mchakato ulianza upya ambapo utaratibu wa ukusanyaji wa michoro, picha ya vazi au mavazi halisi kutoka kwa wabunifu kwa kila mkoa uliandaliwa kwa kuwaandikia Makatibu Tawala wa Mikoa yote, kuwapa taarifa kuhusu mchakato wa kupata Vazi la Taifa kwa kushirikiana na Maafisa Utamaduni kuhamasisha wabunifu ili waweze kuandaa, kuwasilisha michoro, picha au mavazi waliyobuni yanayoendana na asili ya mkoa husika. Aidha, Wizara imeweka mkakati maalumu kwa kushirikiana na Maafisa Utamaduni ili kuweza kupata Vazi la Taifa.
MHE. FELISTER A. BURA aliuliza:-

Serikali ilipata ufadhili wa kujengewa uwanja wa michezo Mkoani Dodoma kutoka Serikali ya Morocco.

Je, ni lini uwanja huu wa Michezo utaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Felister Aloyce Bura, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mfalme Mohamed VI alipofanya ziara yake katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Oktoba, 2016 alitoa ahadi ya kufadhili miradi mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na ujenzi wa msikiti mkubwa na ujenzi wa uwanja wa kisasa wa michezo nchini. Baadhi ya ahadi kama ujenzi wa msikiti zimeshakamilika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ujenzi wa uwanja wa michezo wa kisasa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliamua uwanja huo ujengwe katika Jiji la Dodoma eneo la Nane Nane. Maandalizi yote ya msingi ikiwa ni pamoja na kutenga eneo lenye jumla ya ekari 328.6, kupima eneo lote la mradi, kufanya tathmini ya mazingira na kijamii (Environmental and So cial Impact Assessment), topographical survey, geotechnical survey na kuandaa mchoro wa awali wa uwanja tarajiwa yamefanywa.

Mheshimiwa Spika, kimsingi maandalizi ya awali ambayo yalipaswa kufanywa na Serikali ya Tanzania yamekamilika kwa kiasi kilichokusudiwa. Aidha, mawasiliano baina ya Serikali mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Morocco kuhusu kukamilisha mradi huu yanaendelea.