Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Khadija Hassan Aboud (2 total)

MHE. KHADIJA HASSAN ABOUD aliuliza:-
Je, Serikali imejipanga vipi kukidhi mahitaji ya viuwadudu kwa wakulima wa pamba?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khadija Hassan Aboud, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa viuwadudu katika kudhibiti magonjwa na visumbufu vya mazao nchini.
Katika msimu wa kilimo wa mwaka 2017/2018 wakulima wameitikia kwa vitendo azma ya Serikali ya kuimarisha kilimo cha pamba nchini kwa kuongeza eneo linalolimwa pamba kutoka wastani wa ekari 1,000,000 hadi wastani wa ekari 3,000,000. Kutokana na mwitikio huo, hadi tarehe 22 Desemba, 2017 jumla ya ekari 1,500,000 zilikuwa zimelimwa na kupandwa zao la pamba na kwa kuhitaji chupa zile (acrepacks) 4,500,000 za viuwadudu. Hata hivyo, kwa kuwa mvua zinaendelea kunyesha wakulima wameendelea kuhakikisha kwamba zao hili linafanyika na vilevile suala la viuatilifu linafanikiwa. Nakushukuru.
MHE. KHADIJA HASSAN ABOUD aliuliza:-

Idara ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s) inafanya kazi zake kwa weledi na uadilifu mkubwa lakini haina mamlaka ya kujitegemea kama zilivyo BRELA na RITA.

Je, ni lini Serikali itaipa Mamlaka Idara hiyo kuwa Taasisi inayojitegemea?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khadija Hassan Aboud, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mwaka 2017 Ofisi ya Waziri Mkuu iliandaa kikosi cha kupitia, kuchambua na kushauri juu ya namna bora ya uratibu wa mashirika yasiyo ya Serikali. Moja ya mapendekezo yaliyotolewa ni kuifanya Idara ya Mashirika Yasiyo ya Serikali kuwa Taasisi inayojitegemea. Hata hivyo, suala hilo ni la kimuundo na linahitaji maandalizi ya kutosha. Serikali inatoa rasilimali fedha na rasilimali watu wa kutosha pamoja na vitendea kazi muhimu ili kumwezesha Msajili kufanya kazi yake na umadhubuti chini ya usimamizi wa Bodi ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Serikali. Serikali inayafanyia kazi pasipo kuingiliwa na pia ina wawakilishi wa Serikali na NGO’s.

Mheshimiwa Spika, katika hatua za kuboresha uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Serikali. Serikali imefanya marekebisho ya Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Serikali, Sheria Na. 3 ya mwaka 2019 na kuweka masharti yote ya kusajili chini ya Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Serikali na hivyo kumpa mamlaka mbalimbali Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Serikali ikiwemo kusimamia Shirika husika, kufanya kazi pale linapopatikana na makosa wakati ikisubiri uamuzi wa Bodi. Aidha, mashirika yametakiwa kuwasilisha kwa Msajili taarifa ya utekelezaji ya robo mwaka, taarifa za ukaguzi wa fedha za mwaka na mikataba ya fedha ambayo mashirika yanaingia na wafadhili na kuweka bayana kwa umma taarifa za mapato na matumizi ili kongeza uwazi na uwajibikaji.

Mheshimiwa Spika, nyenzo hizo ni muhimu katika kumfanya Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Serikali kufuatilia utendaji wa mashirika hayo na hivyo kuchukua hatua stahiki. Hivyo kwa sasa Serikali haina mpango wa kuifanya Idara ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Serikali kuwa Taasisi inayojitegemea.