Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mariamu Ditopile Mzuzuri (16 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma mwenye kurehemu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kukushukuru wewe, Mheshimiwa mtani wangu, maana niliona mbona napitwa, muda unazidi kwenda na mimi sipati nafasi. Napenda ni-declare interest, mimi ni mkulima. Tumezoea kusikia mtoto wa mkulima, mtoto wa mfugaji, mimi ni mtoto wa kishua, lakini ni mkulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuanza kwa kusema, naipongeza Tanzania, napongeza Serikali zote za Chama cha Mapinduzi kuanzia Awamu ya Kwanza, ya Pili, ya Tatu, ya Nne na hii ya Tano.
Waheshimiwa Wabunge wenzangu, huu mchezo hauhitaji hasira na msema ukweli mpenzi wa Mungu. Kama wewe unasema tupo nyuma, India wanatambua korosho bora inapatikana Tanzania, dunia inatambua mwaka 2015 kwa mujibu wa FAO kati ya nchi 10 duniani zinazoongoza kwa kuzalisha ndizi, Tanzania imo. Pamoja na yote, tumo kwenye ramani. Serikali zetu zimekuwa zikihangaika na kilimo na zinazidi kuboresha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais, ametuletea wahusika ambao watatuvusha. Nina uhakika kipindi hiki cha 2015 na ninamwomba Mheshimiwa Rais, hii timu wasiibadilishe mpaka tufike 2025; Mheshimiwa Mwigulu na mwenzake watatuvusha mbali sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ya kuyaboresha ili tufike mbali. Cha kwanza ni sera, kwa sababu kuna vitu tunashangaa tu. Leo hii haiwezekani mbegu inayozalishwa hapa nchini iwe inatozwa ushuru mkubwa kuliko mbegu inayoagizwa kutoka nje. Kwa sababu wataalam wanasema, mbegu inatakiwa ifanyiwe tafiti mahali husika. Kuna factors nyingi za hali ya hewa na aina ya udongo uliopo. Kwa hiyo, tukibadilisha hizi sera zetu, namwomba Mheshimiwa Waziri akae chini apitie sera zilizopo, je, zinaendena na wakati? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi zitamsaidia yeye maana kuna watu wameshaanza kumtisha, na mimi nikakumbuka, ametaja baadhi ya Mawaziri ambao walipitia Wizara yako leo hii hawajarudi, nikakumbuka na baba yangu mdogo yumo kipenzi changu Mheshimiwa Adam Malima, na yeye alipita huko hajarudi, lakini nasema kwamba Mheshimiwa Mwigulu utaiweza na itakufikisha sehemu ambapo wewe unapaota, angalia hizi sera! (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja limechangiwa sana na watu hapa, mimi ni mwana maendeleo, ni kijana, ninalinda interest ya kundi kubwa ambalo lina-constitute hii nchi. Kuna watu mnawasema vibaya, jamani wafanyabiashara wamo humu, kuna biashara ambayo haina channel of distribution? Kwenye biashara lazima una producer, una mtu wa katikati ambaye anapeleka kwa final consumer. Kwa nini kwenye kilimo huyu mtu wa kati anapigwa sana vita? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliomba ridhaa kwa Wana-Dodoma hususan vijana kuja kuwawakilisha, mimi mkisema hivyo mnaniumiza. Nina vijana wengi sana ambao wanafanya biashara za mazao na naomba kuwasemea, wanafanya kazi kubwa kuisaidia Serikali kuendesha kilimo. Hawa watu wana-invest kule. Ninyi mnapochelewa kupeleka mbegu, hawa ndio wanaenda kuwapa wakulima mbegu na muda mwingine inaweza kutokea mvua hazijatosha, hawajapata kitu. Hela zao wao ndio zinakuwa zimepotea.
Naomba tuwaendeleze hawa, tuone ni namna gani ya kuimarisha mahusiano baina ya wakulima na hawa vijana wetu. Haiwezekani leo hii tumsifie kijana Mtanzania anayeenda kuchukua nguo China kuja kuuza, tumkandamize huyu ambaye aliamua kufanya kazi na mkulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo mengi, nimeshauri sana tangu niwe Mbunge kwa sababu nina interest na kilimo na ninajua kilimo ndiyo cha kututoa.
Napenda kuzungumzia vijana. Kuna kundi moja la vijana ambao ni wahitimu wa Vyuo Vikuu, imekuwa kwao tatizo ni ajira, lakini wapo ambao wanajitolea, mmojawapo ni mimi. Tangu nilipomaliza diploma niliamua kuingia kwenye kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, lakini hawa vijana kutumia vile vyeti vyao tu kama collateral na Serikali iwasimamie vizuri, waweze kuwezeshwa kufanya kilimo chenye tija na cha biashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukaunda kundi la hawa wahitimu mmoja akiwa mtaalam kutoka SUA mwingine awe accountant, mwingine awe mtu wa procurement, mwingine awe marketing; wakiungana hao wakaenda shambani na ukawawezesha kwa nyenzo, wakaenda kulima, wakauza, watafanikiwa na wao wenyewe watakuwa ni source ya ajira kwa vijana wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo mengi sana ya kuchangia, nitaandika kwenye mchango wa maandishi. Tunataka kumtoa Mtanzania kwenye kilimo cha jembe, Mheshimiwa Mwigulu thubutu na utaweza. Weka sera ya kila kijiji kiwe na trekta. Tuna vijiji 19,200 kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012; ukipiga hesabu ya trekta moja farm track ya milioni 35 na hiyo ni bei ya hapa Tanzania, inakuja hesabu ya kama shilingi bilioni 600.7. Ukithubutu utaweza kwa awamu, sio vijiji vyote vitahitaji! Utaweza na utakuwa umeacha trade mark ambayo haitafutika mioyoni mwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri, kwa kuwa tunataka tuweke uchumi wa viwanda, tufanye kilimo cha biashara. Naomba tuanzishe agricultural zones, ifahamike. Ukanda ambao unalima ndizi, u-concetrate, uboreshe mbegu nzuri za ndizi ambazo tutaweza ku-export. Tunaweza kwenda Bukoba na Mbeya hawa wakawa zones za kulima ndizi, machungwa kwa watani zangu Tanga, mananasi kwa watani zangu Wasukuma Geita, pamoja na kwa kaka yangu Mheshimiwa Ridhiwani, ikawa ni zone kwa ajili ya mananasi. Tuna kilimo cha maua, leo hii Songwe, Mbeya, Iringa Arusha na uzuri miundombinu ipo, kuna airport, we can export fresh flowers to Europe and elsewhere in the world. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirudi kwetu Kanda ya Kati tukazanie kwenye alizeti, ufuta, choroko, dengu, mbaazi and I tell you Tanzania ni nchi ya tatu katika Afrika ku-produce mbaazi. Tunatengeneza mbaazi nzuri kweli! Mpwapwa kwa Mzee Lubeleje ndio wanatengeneza the best karanga in the world ambayo inatoa mafuta mazuri. Kwa nini tusitumie fursa hii kwa ajili ya kupata kipato kikubwa katika nchi yetu?
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Kwa hiyo, nashukuru sana. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi kuweza kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja naomba nilitolee ufafanuzi. Serikali iliyokuwepo madarakani ni Serikali ya Chama cha Mapinduzi; Serikali ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi na inatekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015/2020. Sasa leo hii unatofautishaje Serikali ya Chama cha Mapinduzi na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Awamu ya kwanza ilikuwa ni ya CCM, ya pili ya CCM, ya tatu ya CCM, ya nne ya CCM na ya tano ya CCM. Leo hii Mheshimiwa Rais Magufuli akizindua kiwanda ambacho jiwe la msingi liliwekwa na Kikwete hapo kuna tatizo gani? Maana watu wanaleta hoja ambazo hazina mashiko. Tumepewa nafasi hii kutoa michango naomba tutoe michango ambayo inaleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mdogo tu mimi Mzaramo nitatoa mfano, leo hii kaka yangu Kubenea ameenda kuoa baada ya harusi akitembea na mke wake watu watamsifu, Kubenea una mke mzuri, alimlea yeye? Ni kwa nini wasisifie wazazi waliomlea yule mke. Nimetolea
mfano, utapewa sifa wewe mume wa yule mke ingawa hujamzaa wala hujamlea wewe. Kwa hiyo, mafanikio ambayo leo hii tunajivunia ya awamu ya tano yanatokana na misingi mizuri ya Chama cha Mapinduzi na Serikali zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alivyokuwa anaomba ridhaa ya kuongoza nchi hii wimbo wake mkubwa ulikuwa kwamba tutajenga Tanzania yenye viwanda na ninampongeza. Mheshimiwa Rais ameanza kuweka mikakati ya kitaifa ambayo itatupeleka kwenye uchumi wa viwanda. Uwekezaji kwenye reli ulio kwenye kiwango cha standard gauge, kinaenda kuwekeza kwenye uchumi wa viwanda. Ununuzi wa ndege ambao tunafufua Shirika letu la ATCL leo hii lazima tutambue tunasafirisha minofu ya sangara kwenda nje ya nchi, tunasafirisha maua, tunasafirisha mboga mboga. Leo tumeanza kununua ndege za abiria ndogo mpaka kubwa, najua huko mbele tutaenda kununua ndege za kusafirisha mizigo. Kwa hiyo, zile bidhaa zetu tutazisafirisha kwa shirika letu, tuta-enjoy economies of scale. Kwa hiyo, lazima tutambue kwamba uwekezaji huu kwamba Mheshimiwa Rais anasimamia kauli yake na kwa level yake ya juu kabisa ameonesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye uwekezaji wa Stiegler’s Gorge kwenda kuzalisha umeme yote hii tunaona kwamba tunaenda kuelekea kwenye uchumi wa viwanda. Waliokuwepo chini ya Mheshimiwa Rais, Waheshimiwa Mawaziri hususani Waziri Mwijage, kama uthubutu wa Mheshimiwa Rais kuwekeza kwenye haya mambo je, wewe unaendana naye? Kila saa anasimama Mheshimiwa Rais kuwaambia wasaidizi wake hivi kweli mnaelewa mimi ninayoyahitaji? Je, mnasoma mimi nini ninachokitaka? Tunakuomba Mheshimiwa Mwijage lazima ujiulize mtu akikusifia makofi matatu hayazidi. Kwa hiyo, je, unaendana na ajenda? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba, mimi nina neno moja kwa Mheshimiwa Waziri naomba uwe serious kwenye hii ajenda ya viwanda na uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu tunaenda kujenga viwanda na viwanda tayari vipo vya ndani tunavilindaje? Maana kuanzisha kiwanda ni jambo moja, lakini kuvifanya viwanda hivi viwe endelevu na vizidi kukua lazima tuweke ajenda muhimu je, Mheshimiwa Waziri naomba ukiwa unakuja kujibu hoja utuambie una mipango mikakati gani gani ya kulinda hivi viwanda ambavyo tunavianzisha? Unaweza ukaanzisha viwanda vikatoa bidhaa visinunulike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunawaambia wananchi wetu tuwe wazalendo tununue bidhaa za ndani, lakini unaweze ukakuta nguo kutoka China ina bei nafuu kuliko nguo iliyotengenezwa Mwatex na haya matatizo tunasababisha wenyewe, viwanda vya ndani vinaonewa, urasimu ni mwingi, umangimeza umejaa, utitiri wa kodi na usumbufu ambao hauna sababu. Mwenye kiwanda atafuatwa Halmashauri, atafuatwa na Mbunge, Diwani, OSHA na Wizara, yaani imekuwa ni usumbufu. Tunawaambia wawekeze hela, tunawapa pressure katika kurudisha mitaji yao na kuweza kujiendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano mdogo, leo hii mtu akileta nyuzi ama nguo kutoka nje ya nchi, ataleta estimates za uongo atawekewa kodi ndogo, lakini huyu mwenye kiwanda ndani atakuwa charged kodi nyingi, hatimaye cost of production inakuwa kubwa anashindwa kufikia break even, anafeli. Kwa hiyo, lazima tuangalie na tuwe na mikakati. Naomba na nasisitiza ukiwa unajibu hoja unijibu kwamba una mikakati gani katika kulinda hivi viwanda na uwekezaji wa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu chochote lazima kiwe na washika dau. Waheshimiwa Mawaziri wote kwa ujumla hasa Waziri wa Viwanda, jamani msiwaogope wafanyabiashara na wawekezaji, hii inaenda kwenu Waheshimiwa Mawaziri na watendaji, mfanyabiashara ataomba appointment na kuonana na Waziri au mtendaji mtamkwepa, mnamkwepa nini. Yule ndiye mdau wako, kaa naye ujue changamoto zake na yeye umueleze mambo na mikakati ya Serikali. Utapigiwa simu na mwekezaji aah naogopa, hutaki kumuona wa nini? Utapata wapi information za kukusaidia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mtu mla rushwa atakuwa mla rushwa tu, rushwa zina aina nyingi sana kupatikana, kwa hiyo, tusiwekewe hawa watu. Pia nikupongeze MheshimiwaMwijage maana naona jana ulialika wadau wako wamiliki wa viwanda akiwemo Mzee wangu Kilua mmiliki wa Kilua Group. Kwa hiyo, hilo nalo nikupongeze, lakini wengine wote tusiwaogope hawa ni wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema when government walks, business community runs. Kwa hiyo hawa ni wadau wetu tusiwakwepe, tukae nao tujue changamoto tuweze kusaidiana kupeleka gurudumu la maendeleo mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala naomba niliweke vizuri na na-declare interest kwamba mimi ni mkulima na ni mchuuzi wa mazao. Kwa hiyo, nikiongelea natafuta soko la ufuta nafuatilia kwenye soko la dunia na vilevile nchi za wenzetu hali yao ya kuvuna, maana lazima tuelewe si Tanzania peke yake duniani ndiyo inayolima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa tu mtambue kwa mujibu wa FAO, India ndiyo nchi ya kwanza inayolima mbaazi duniani, lakini India ndio nchi ya kwanza ambayo pia inanunua mbaazi duniani. Yote ni kwa sababu India ndiye mtumiaji wa kwanza wa mbaazi, tofauti na chakula India anakamua mbaazi mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichotokea msimu wa mwaka 2017/2018 kuhusu mbaazi maana shutuma nyingi zinakwenda kwa Serikali, penye kushauri tushauri ukweli, penye kukosoa tukosoe ukweli na kwenye kusifia tusifie ukweli. I am talking because I know. Mimi nilikuwa nafuatilia suala la mbaazi, kilichotokea msimu uliopita India ili-over produce mbaazi. (Makofi)

Mimi nilikuwepo kule na nikaenda Lower House Bungeni kwao na siku hiyo nilikuta mjadala Wabunge wa Upinzani wamewachachamalia Serikali wakiwaambia najua mmeenda nchi za Afrika ikiwemo Tanzania mmekubaliana kwamba mta-import mbaazi kutoka kwao, sasa wakulima wetu wamelima hawana soko, tunaomba muweke ban kwenye importation ya mbaazi kutoka nchi za Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tuliaothirika sio Tanzania peke yake ni pamoja hata na jirani zetu Malawi ambao wanalima kuliko sisi. Kwa hiyo, sasa usiwe wimbo wa kuikosoa Serikali; mnyonge mnyongeni haki yake mpeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndiyo maana naunga mkono jibu la Naibu Waziri alilosema kwamba hata na sisi tujifunze kula mbaazi, sisi ni Wabunge tumeaminiwa lazima tujiongeze kwenye kudadavua mambo, hajamaanisha ukapike nyumbani kwako, tu-cultivate tabia ya sisi wa kwanza kutumia bidhaa tunazozizalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikaenda mbali nikasema ili Serikali muwe mfano, basi kule magerezani na mashuleni tunapeleka vyakula tuwafundishe kule kula mbaazi instead of maharage ili ninyi muanze kama mfano. Sisi tunapoenda Mjimboni mwezi mtukufu wa Ramadhani watu mnaongelea mafuta, sukari tuseme na mbaazi, hata kiafya ni nzuri. Kwa hiyo, lazima sisi tuwe mfano, bidhaa zetu sisi tuwe watumiaji wa kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ndicho kinachotukuta, ufuta wote tunautoa nje kwa sababu hatujui umuhimu. Unaambiwa duniani hata hii alizeti tunaongea cholesterol free it’s not true, mafuta ambayo hayana rehemu kabisa ni mawili, mafuta ya ufuta na mafuta ya nguruwe (pig fat), that is the truth. Kwa hiyo, leo hii tunasafirisha ufuta wote kwenda nje kwa sababu hatupo aware kuhusu... (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi naunga mkono hoja nawashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii kuweza kuchangia kwenye hoja iliyoko mezani ya Bajeti ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niungane na wenzangu wote kwa pongezi walizotoa kuanzia kwa Mheshimiwa Rais wetu pamoja na viongozi wetu kwenye Wizara. Babu yangu Tabasam ametangulia kumpa angalizo Mheshimiwa Ulega kwamba yeye ni mzoefu kwenye Wizara hii na siyo mgeni na sasa ana mamlaka iliyokamilika kwa hiyo tunategemea makubwa sana na wewe ni kijana mnyenyekevu msikivu. Kwa hiyo, natumai hata Mheshimiwa Mhagama amekwambia ukitusikiliza Wabunge basi haya mambo uliyoyapanga yatafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri kwenye maeneo machache; la kwanza ni takwimu. Hivi tunavyoimba kwamba tuna ng’ombe milioni 32 tuna bata 10,000. Ni mfumo gani ambao umeutumia kutupa data hizi? Sitaki kuongea sana kwa undani lakini ushauri wangu sijui mfumo gani maana yako hayo mambo ya hereni na nini yanapigiwa kelele. Kama nia ni njema lakini huo utaratibu kidogo una ukakasi rudi nyuma kwa sababu huwezi kukamilisha mipango yako kama huna takwimu sahihi. Huwezi kwenda huko unakotaka kwenda kama hutokuwa na takwimu sahihi, una kaya ngapi zinazojihusisha kwenye mifugo na aina ya mifugo kwenye kaya hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kwa kweli kwenye mipango yote anza na takwimu ndiyo itakuwa ufunguo mzuri wa wewe kwenda mbele kwenye mipango yako. Mheshimiwa Waziri kwa kweli hebu pitia upya sera zako pamoja na sheria mbalimbali kwenye mifugo na uvuvi. Leo hii kelele zote tunazopiga Waheshimiwa Wabunge kumshauri huyu anatumia Sera ya Mifugo ya Mwaka 2006, kweli Mheshimiwa Waziri? Tuko mwaka 2023 Sera ya Mifugo tunayotumia ni ya 2006. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii unatumia Ilani ya Uchaguzi ya 2020/2025, unatumia Mpango wa Taifa wa Maendeleo 2021/2026. Kweli hii sera yako ya mifugo ya 2006 itakupeleka unakotaka kwenda? Kwa hiyo, ni vyema hebu tuweze kupitia hizi sera zetu. Pia kuna sera nyingine kati ya chache ambazo nataka kutolea mfano, kuna policy inaitwa disease control policy (Sera ya kupambana na kudhibiti magonjwa yatokanayo na mifugo na mazao ya mifugo). Kama hatutoweza kuipitia hii kitu kwa kweli ndoto ya sisi kuuza bidhaa zetu kwenye soko la kimataifa tulifute.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mfano ambao uko hai. Kuna kampuni siitaji jina ilipata soko kubwa la nyama ambayo imechakatwa kwenye thamani mbalimbali kule Afrika Kusini pamoja na Nchi ya Msumbiji. Walikwama kwenye soko hilo kwa sababu leo hii nyama yetu hairuhusiwi kuuzwa kwenye nchi za SADC kwa sababu tunao ugonjwa wa foot and mouth disease. Siyo kwamba huo ugonjwa hamuufanyii hatua za kuudhibiti lakini policy yetu ya disease control haiko wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wafanyabiashara wengi hawasemi tu, hata hao wanaotafuta soko la maziwa, soko la nyama za kuku huko nje, mayai wanakutana na hichi kitu. Maswali wanayoulizwa hawana majibu sahihi. Kwa hiyo mimi naomba sana Mheshimiwa Waziri hebu hizi sera zetu twende tukazipitie, sheria zetu lete hapa zifanyiwe marekebisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunaongelea blue economy lakini nautical miles zinazoruhusiwa kuvua samaki haziwezi kuleta tija siyo tu kwa wavuvi wadogo, hata kwa wawekezaji wakubwa wenye viwanda vya samaki haiwezi kutuletea tija Mheshimiwa Waziri. Naomba hizi sheria kaa uzipitie na wataalamu wako, tuletee hapa Bungeni tuweze kuzirekebisha na kuzipitisha ili hicho unachopanga kwenye mafanikio yako iweze kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri unataka kwenda kuongeza kipato kwenye sekta hii na wako Waheshimiwa Wabunge waliotangulia wanashangaa Sekta ya Uvuvi siyo ya kuchangia 1%, hiyo ni aibu. Hebu jiulize leo nchi zinazotuzunguka tunawapelekea mahindi na bidhaa za kilimo kwa nini siyo bidhaa za uvuvi ama za ufugaji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwennyekiti, tuna ng’ombe wengi kuliko nchi za jirani. Leo hii Tanzania tumezungukwa na land locked countries ambazo hawana bahari lakini kwenye maziwa matatu tuliyokuwa nayo, Victoria, Tanganyika na Nyasa sisi ndiyo wenye share kubwa ya hayo maziwa kuliko nchi jirani. Kwa nini sisi tunashindwa kutumia hii kama fursa ya kuweza kujiongezea kipato lakini kuna mambo ambayo yanakuwa kikwazo kwenye hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni biashara ya haya mazao yetu mengi yanafanyika kwenye mfumo usio rasmi. Mfano, soko la maziwa, 97% ya maziwa yetu yanauzwa kwenye mfumo usio rasmi, ni 3% tu sasa hapo utaonaje tija ya biashara ya maziwa kama haujaimarisha kwamba haya maziwa yanayozalishwa na wafugaji wetu yakauzwa kwenye mfumo ambao ni rasmi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Tabasam ametangulia kusema anasikitika Ziwa Victoria lile tunaenda kuwa nalo ambalo halina tena mantiki tena babu zangu Mwanza kule bahati nzuri zamani walikuwa na dhahabu, sasa hivi dhahabu imehamia Geita. Sasa Mwanza hii miaka kumi na kitu iliyopita tulikuwa tuna viwanda zaidi ya 10. Leo Mwanza vimebaki viwanda vitatu tu vya kuchakata samaki.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mariam kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Amar.

TAARIFA

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa mzungumzaji kwamba hatuwezi kuwa na tija kwa wafugaji wetu kupata maziwa yaliyo mengi kwa sababu tuna maafisa ugani wachache. Mfano Nyang’hwale tuna maafisa ugani wako wanne na tuna kata 15 na kuna wafugaji unamkuta ana ng’ombe 100 lakini hata lita tano za maziwa hazipati. Hatuwezi kufanikiwa kwa mtindo huu. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana, Mheshimiwa Mariam taarifa unaipokea?

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea na pia niunge mkono hoja ya Waziri ya kutaka kuanzisha hizi mamlaka maalum ili zitamuongezea rasilimali watu lakini na rasilimali fedha. Kwa hiyo rai yangu kwa Serikali hii mipango ya Waziri basi wakaipokee na waweze kumpa fedha ili aweze kuikamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii niwaambie hatuwezi kuona tija na thamani ya sangara kama hatutopeleka sangara kwenye Soko la Dunia. Sangara akiuzwa kwa mama ntilie hapa ndani ya nchi hana tija na Waziri unajua. Sangara ana vitu viwili; ana mnofu, ana kitu kinaitwa mabondo (fish morse) lakini nisikitike leo viwanda vimeenda kufa ajira zimepungua kwa sababu tu hii biashara ya mabondo inafanywa kiholela. Unapoteza mapato Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikwambie hebu kunja moyo fanya maamuzi magumu. Hebu tuombe ndani ya miezi mitatu au miezi sita, rasimisha hii biashara, mtu hakatazwi kuuza mabondo yake lakini aende akauze kwenye sehemu ambazo zimeidhinishwa na wizara, kama viwandani na center zingine za kupokea kwanza utafanya udhibiti wa thamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu hakatazwi kuuza mabondo yake lakini aende akauze kwenye sehemu ambazo zimeidhinishwa na Wizara, kama viwandani na center zingine za kupokea. Kwanza utafanya udhibiti wa thamani; leo hii hayo mabondo yenyewe siyo kwamba yana grade moja, mabondo yana grade A, B, na C. Leo hii wewe huna hiyo takwimu, mabondo unauza tu kama bondo, leo hii mimi najua…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mariam.

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo una mipango mikakati mizuri ya kuzalisha sato. Leo hii sangara ana bei ndogo kuliko sato. Hao sato unaowazalisha watakosa soko kwa sababu sangara yuko humu ndani, wakati sangara tukimtoa nje ataleta tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kumalizia, ninao ujumbe kutoka kwa wananchi wa Jimbo la Kondoa Mjini, wanakusifu sana Mheshimiwa Waziri unafanya kazi kubwa wana maombi mawili. Machinjio yetu kule…

MWENYEKITI: Muda wako umeisha.

MHE. MARIAM D. MZUZURI: … kwa kweli yamechoka na hayakidhi usalama wa ng’ombe wanaochinjwa pale pia ni wafugaji wakubwa wa kuku wa kienyeji. Faida za kuku wa kienyeji tunazijua, tunaomba utuletee wawekezaji ili…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. MARIAM D. MZUZURI: … ufugaji ule wa kuku wa kienyeji uweze kuwaletea manufaa wananchi wa Kondoa Mjini, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi niweze kuchangia katika hotuba yetu hii ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Kwanza nipende kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na timu yao katika wizara kwa yale ambayo wameweza kufanikiwa kuyafanya ambayo bado yapo kwenye mchakato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mwana CCM na huwa nikipenda kushauri ukweli napenda kutumia kati ya moja ya ahadi zetu za uanachama, nitasema ukweli daima fitina kwangu mwiko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya upatikanaji wa Sangara katika Ziwa Victoria ni mbaya sana; sasa sijajua kama kwenye vipaumbele vya wizara yetu hii wameliona hili na kulitaka kulitafutia ufafanuzi. Kwa nini nasema hali mbaya? Sangara ni bidhaa kubwa sana katika Soko la Samaki la Export katika dunia, Europe ndiyo soko kubwa sana ambalo zaidi ya asilimia 70 ya mazao ya Samaki yanayotoka Afrika yanakwenda huko Europe, zaidi ya asilimia 70. Mwaka 2014/2015 Tanzania tulikuwa tunatoa zaidi ya tani 45,000 za minofu ya Sangara na mazao yake; lakini mwaka 2021 tumetoa tani 14,000 tu; lakini viwanda vyetu vilivyokuwepo mwaka huo 2014/2015 tulikuwa tunaajiri zaidi ya vijana 12,000 kwenye sekta hii. Nasikitika kusema ajira imepungua zaidi ya asilimia 50 na leo hii tuna takriban vijana 4,000 tu ambao wameajiriwa kwenye sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Wabunge wa Mikoa ya Mwanza na Jirani ni mashahidi, ukienda kuhoja wamachinga waliokuwepo mtaani, miaka kumi kumi na ngapi nyuma wengi walikuwa waajiriwa kwenye viwanda hivi; Lakini hapo zamani viwanda vilikuwa vinafanya kwa siku shift tatu na vilikuwa operational wiki nzima siku saba ndani ya wiki; lakini cha kusitika hali sasa hivi viwanda hivi vinafanyakazi kwa shift moja na nusu kwa siku na siku nne tu kwenye wiki. Kwa hiyo, nimetoa picha hii ili tujue leo royalty inakuwa inapatikana kwenye biashara ya sangara ndiyo ilikuwa inasaidia kuleta maendeleo kwenye nchi yetu; ilikuwa inasaidia kujenga hospitali, Vituo vya Afya na maeneo mengine ya kimaendeleo katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa nimeangalia sana hotuba ya Mheshimiwa Waziri bado sijaona. Ninaamini jambo ambalo linasababisha hali hii ni uvuvi haramu. Lakini nimesikitika kuona kwamba katika vipaumbele vya wizara sijaona palipoandikwa kwamba mna mkakati wa aina gani madhubuti wa kupambana na uvuvi haramu. Lakini naweza kutoa tu maoni na kama mnayafanyia kazi mmesahau tu kuandika mtanitolea majibu huko wakati mnajibu hoja zangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niulize Mheshimiwa Waziri nimefuatilia unazo takwimu kweli kuhusu viwanda ambavyo uko navyo, kwa sababu kati ya wageni mliowaalika wamiliki wa viwanda kuja kuhudhuria bajeti hii, mmewaalika Kampuni inaitwa Prime Catch lakini hii Prime Catch imefungwa miaka 10 iliyopita hakipo hiki kiwanda; kuna kiwanda kinaitwa Vick Fish, hakipo kilishafungwa hiki kiwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Uganda ambayo inasehemu ndogo sana ya Ziwa Victoria inatuongoza kwa kuwa na idadi ya viwanda vingi kuliko sisi; Leo hii kwenye nchi 10 Afrika zinazopeleka minofu ya Samaki kwenye soko la dunia Tanzania hatupo; Uganda ambao ni landlocked country inayo Ziwa Victoria peke yake haina ukanda wa Bahari kama wa kwetu ipo ni nchi ya 10 Afrika. Sasa naongea hivi kwa masikitiko makubwa sana, yapo maeneo Mungu ametubariki mno, kikubwa ni utashi wa kutambua tatizo lipo wapi tukapata uthubutu wa kushughulikia hili tatizo ili kunusuru hali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka niulize huko nyuma kuna operation ilianzishwa kwa ajili ya uvuvi haramu, al-maarufu operation Sangara, nia ilikuwa njema lakini niulize kama wizara je, mnayo tathmini ya operation kwa sababu kwa wananchi leo ukiwauliza kuhusu operation hii ni majeraha matupu. Operation iliyokwenda kutia umaskini watu, iliyosababisha vifo kwa watu kupata mapresha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sijui kwa upande wenu Serikali tunaomba mje na tathmini je operation hii ilikuwa na manufaa gani kwa nyie mnavyoona huko; na je mlichopanga kufanya kikaende ndivyo sivyo mnarekebishaje ili basi tuweze kuwa na mipango Madhubuti, kwa sababu nimesoma gazeti la Guardian la tarehe 20 Mei, 2022; Wizara mlitoa kauli kwamba mmejipanga kuwekeza fedha nyingi kwa ajili ya kupambana na uvuvi haramu. Sasa nataka kuliko kwenda kulitia tena Taifa kwenye hasara tujue ile operation ilifeli wapi, hasara ilikuwa wapi, ili kabla hamjachukua fedha hizi za umma kuziingiza huko tayari muwe na tathmini na tujue mmejipanga vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri unao maafisa wetu wa uvuvi katika kila nyanja kwa maana ya vijijini mpaka mikoani. Tumewaweka hawa kule kwa ajili ya kusimamia hizi rasilimali zetu kama vitendo hivi vinaendelea inamaana wao wanaviruhusu; wao ndiyo wapo kwenye mialo, wao ndiyo wapo kwenye catchment area; Je, mmewawajibisha vipi hawa wanaosimamia hii rasilimali iwe ya kinidhamu ama kiutendaji, je wanawaletea ripoti, hizo ripoti mnazifanyia kazi, je kama ni uzembe wao mmewachukulia hatua gani tuanze nao hao ili watatupa majibu mazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hongereni mmechukua hatua ya kukaa na wadau kwa maana ya wavuvi wadogo, wakubwa lakini na wamiliki wa viwanda. Tujiulize kila mmoja yuko bitter kwenye suala la uvuvi haramu, wote wahusika wako bitter. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hebu tukae chini tena kama kila mtua anachukia Serikali, wananchi wanachukia, wadau wanachukia shida ni nini Uvuvi huu haramu unaendelea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tunaona katika Ziwa Victoria tunali-share na majirani zetu kwa maana ya Uganda na Kenya na tunaona Uganda ndiyo inaongoza na Uganda ndiyo ina control bei, ina maana leo Uganda ghafla kwa vile wao ndiyo wameshika soko wanashusha bei inakuja kuathiri. Je, mmejipangaje kama Serikali katika kulinda hawa wavuvi wetu wasipate hii athari; cha kwanza kwa kukaa chini na hizi Jirani, kuona kama tunaweza kuwa na bei elekezi ili haya mabadiliko ya kiholela yasiathiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mjifunze kutoka Wizara ya Kilimo, leo hii wamekuja na bima kwa ajili ya wakulima wao kwa nini na sisi tusione namna ya kuwa na bima ya hawa wavuvi wetu ili hali inapotokea waweze kukaa vizuri lakini pia muone namna gani tunaweza kuwa na soko la uhakika; kuliko mtu anakwenda huko usiku kucha yupo gizani anavua halafu akirudi bei imeshuka na inakuwa hasara kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasema tunalo Ziwa Tanganyika, dagaa zinazopatikana Ziwa Tanganyika ni dagaa ambazo ni nzuri haijawahi kutokea. Lakini nasikitika kusema mpaka leo biashara ya dagaa hizi ni kiholela; leo Ziwa Tanganyika, Rukwa, Katavi, Kigoma hakuna kiwanda kikubwa cha Samaki na ukiacha dagaa kule kuna Samaki nzuri, kuna migebuka, tunazo kuhe wanaita kuku wa ziwani, Serikali imejipangaje katika kuvutia uwekezaji wa kiwanda kikubwa kwenye Ziwa Tanganyika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hamna taarifa ninayo, wako wawekezaji wanaotaka kuweka kiwanda kule lakini tangu waanze mchakato imekuwa mchakato mpaka mchakato. Fuatilieni, mjue kama kuna engagement Serikali muwasaidie basi wananchi wetu waweze kuongezewa thamani ya mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tuna mpango wa kuanzisha viwanda kwenye ukanda huu wa Bahari, kwamba kutoka Dar es Salaam mpaka Mtwara, Tanga huu ukanda wote. Miaka sita iliyopita nataka niulize je kipindi chote tangu tuanze kujinasibu na Tanzania ya Viwanda hasa kwa maeneo ambayo tunatumia rasilimali zetu; kwenye ukanda huu wa Bahari kuna kiwanda kipya kimeanzishwa mpaka leo; na kama hakijaanzishwa ni kwa nini; kwa sababu taarifa nilizokuwa nazo ni viwanda kufungwa tu sasa sijui inawezekana hatuna huo ufahamu basi wakati mnajibu hoja mje mtuambie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu tuanze adhma hiyo ya kuanzisha viwanda kwenye ukanda ule, viwanda vingapi vimeanzishwa na vina hatua gani, kama havijaanzishwa sababu nini, na tunajipangaje? Kwa sababu haiwezekani leo hii Morocco ambaye ana sehemu ndogo tu ya Bahari atuzidi sisi kwa ku-export mazao ya Seafood kwenda nje ya nchi, kwa kweli tunamkosea Mungu, Mungu ambaye ametubariki sisi eneo kubwa sana la Bahari. (Makofi)

MWENYEKITI: Kengele imelia Mheshimiwa Mariam.

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi napenda tu leo nimechangia kwa utulivu na hisia kwa sababu kama wizara hatutoweka mipango madhubuti katika kunusuru hali ya bahari na maziwa yetu yakaleta tija kwa Taifa, tutakuwa tunamkosea sana Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan ambaye ameonekana ni mtu mwepesi, msikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo tulikuwa tunapiga kelele kuongezewa bajeti miaka yote lakini bajeti imeongezeka; kwa kweli niwaambie kweli wizara hii mmeniangusha, hotuba hii haijanigusa, naomba kama mna majibu ambayo kidogo yataamsha ari yangu na kuwa na matumaini mapya mje nayo wakati mnahitimisha mjadala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia kwenye bajeti ya Wizara yetu ya Nishati. Kwa kuanza kabisa bila ya unafiki napenda kutoa pongezi zangu za dhati kwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa maana ameonekana kuwa mwepesi sana kujibu hoja na kufanya maamuzi mazito na magumu kuhusu masuala ya nishati. Tumemuona Mheshimiwa Rais tangu Oktoba - Novemba aliruhusu baadhi ya tozo ziweze kutolewa kwenye mafuta ili kuleta unafuu katika bei ya mafuta ambayo imekuwa ikipanda kila mwezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeona namna gani baada ya Bunge kuomba unafuu wa bei kwa ajili ya kuweka maisha mazuri kwa wananchi wetu ameweza kutoa kwa kujibana matumizi yake Serikalini Bilioni 100 kama ruzuku na tumeona matokeo yake mwezi huu bei zimeshuka lakini pia tumeona akitoa maelekezo kwa Wizara ya Fedha na ninaamini Waziri wa Fedha yuko hapa na punde si punde atakuja kutuletea Bajeti Kuu pamoja na marekebisho ya Sheria za Forodha kwa kuleta upungufu kwenye baadhi ya tozo ambazo zitaweza kutolewa kwa ajili ya nishati hii ya mafuta. Kwa hiyo, ninapenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuwa mwepesi kutoa maamuzi ambayo yanaleta unafuu kwenye bei za mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeona namna gani anaguswa na sekta hii na anataka mapinduzi makubwa katika sekta hii ndiyo maana Mheshimiwa Rais ametulia sana kwenye teuzi zake za wataalam na Mawaziri kwenye Wizara hii. Mimi nilipata ukakasi mkubwa sana kwa baadhi ya watu walipobeza uteuzi wa Mheshimiwa Rais kumteua January Yusuf Makamba kuongoza Wizara hii. January namfahamu vizuri tangu naanza ufahamu wa akili ni Kiongozi Kijana ambaye ni kielelezo kwa vijana wengi ambao tuko nyuma katika siasa. Kama hamumjui January Yusuf Makamba ndiye kijana aliyehusika kuandika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi 2015/2020 ambayo Ilani hiyo ndiyo imetuletea ushindi mkubwa wa kihistoria kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2020.

Mheshimiwa Spika, nitasema alama yake kubwa mbili tu alizoziacha kwenye baadhi ya Wizara alizoziongoza, alipata nafasi ya kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, waswahili wanasema mzigo mzito apewe Mnyamwezi lakini mzigo mzito alipewa Msambaa na akauvusha, alipewa kwenda kufuta mifuko ya plastic ili kunusuru mazingira yetu January aliweza na alama ameiweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili alipewa mzigo mzito wa kufuta viroba kwenye nchi yetu, viroba havipo na tunaona afya za vijana wetu zikiimarika baada ya viroba hivi kuondoka. Kwa hiyo sina mashaka na weledi…

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Taarifa.

MWENYEKITI: taarifa.

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kumpa taarifa mchangiaji anayeendelea kutoa mchango wake ni mzuri sana hasa Bilioni 100 zilizotolewa kwa ajili ya kupunguza makali kwa wananchi wale wadogo lakini cha kushangaa bado nauli hazijashuka bei kwa hiyo tuendelee kuishauri Serikali ili kusudi wananchi waweze kufikia ile hatima ya Mheshimiwa Rais aliyokusudia. Ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mariam Ditopile, unapokea taarifa?

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea taarifa nia yake ni njema. Kwa hiyo, nilikuwa namalizia kusema kwamba Mheshimiwa January Yusuf Makamba nimefuatilia mjadala tangu jana ulipowasilisha bajeti yako, kila Mbunge anayeinuka anakusifia na tayari wamekuelewa na wameahidi kwamba wanaenda kupitisha bajeti hii kama kipimo, basi mimi nakwambia Mheshimiwa Waziri tunakukopesha imani sisi kama Wabunge wenzako, kailinde hii imani na ukawatendee haki wananchi wa Tanzania katika sekta ya nishati na sina mashaka kwa sababu unae msaidizi mzuri, kijana mwenzako, Wakili Msomi na umemkuta hapa kwenye Wizara hiyo, kwa hiyo naona kwa umoja wenu mtashirikiana vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye teuzi hizi za Mheshimiwa Rais amemleta Katibu Mkuu ambaye anaijua hii Wizara, nani asiyemjua Mramba katika sekta ya nishati? Pia amemsindikiza Mramba na Msaidizi wake kaleta kijana mdogo Maimbali yuko vizuri amekulia kwenye mfumo kwa hiyo ninaimani kwamba katika Wizara kwa kweli huko chini mjipange mna uongozi wa juu ambao wana dhamira njema na wanaielewa hii sekta vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais hakuishia hapo tumeona teuzi zake za wenyeviti wa Bodi kuanzia TANESCO, REA analeta watu ambao wanaelewa nini wanaenda kukifanya. Hakuishia hapo pamoja na Wakurugenzi, leo hii Ndugu Maharage tumeona namna gani ameiwakilisha nchi kwenda kufanya makubwa nje ya Tanzania kwenye mashirika makubwa ambayo yapo significant ndani ya dunia hii, kwa hiyo amekuja nyumbani kuja kuvusha Shirika letu la TANESCO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitachangia kwenye maeneo machache sana, Mheshimiwa Waziri umetuletea bajeti yako ambayo mimi naichukulia kama ni action road map katika kufikia maono ya Wizara. Kiukweli umetupa mpaka vipaumbele vyako lakini umekuja na ideas mpya kusema kwamba namna gani utaihusisha private sector ili kujipunguzia mzigo lakini namna gani utapata fedha nje ya fedha kutoka Serikali Kuu ili uweze kuendesha mashirika na kuweza kuleta maendeleo katika Wizara yako. Kwa hiyo, mimi nakutakia kila la kheri na tumeona kabisa namna gani unaenda kutekeleza mambo yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu TANESCO ninakupongeza sana Mheshimiwa Mkurugenzi Mkuu tangu uingie umeanza kuonyesha kile ulichokuwa unakifanya namna gani unataka kuki-impact ndani ya TANESCO kwa mambo mawili tu ya mabadiliko ya haraka, ni-connect umeianza kwa muda mfupi lakini tayari wananchi wameishaipokea very positively. Kuna hizi mita janja kwa sababu ilikuwa ni kitu cha ajabu unachukua simu unaigiza mita unanunua umeme tena uende ukatafute pa kuweka zile mita lakini yote ina-portray ni namna gani una maono makubwa ya kuja kubadilisha Shirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili Shirika ni kubwa lina na sehemu tatu kuu ambazo ni kubwa sana lakini nina uhakika kwa timu uliyonayo mtaweza kutekeleza yale ambayo mmeyakusudia na mwisho wa siku kweli mkasadifu ile kauli ya kuliangaza Taifa. Tumeona shida kubwa ambayo inatutatiza ndani ya TANESCO ni kukatika kwa umeme. Mimi naomba nitoe ushauri wangu msichukulie kukatika kwa umeme kwamba ni kadhia tu kwa wananchi na watumiaji wa umeme. Pamoja na huduma mnazotoa TANESCO mnafanyabiashara ya umeme. Mtu anatumia umeme regardless ni wa TANESCO ama ni wa generator sasa kile kipindi ambacho umeme umekatika yule mtu anaenda kutafuta source nyingine ya kutumia umeme, ina maana nyie mnapoteza mapato. Hata hapa Mheshimiwa Waziri wa Fedha upo CAG anapoenda kufanya ukaguzi kwenye mahesabu ya Shirika hili, aende akaangalie ule muda ambao TANESCO umeme umekatika mapato wanayopoteza. Kwa hiyo, nimeona dhamira nzuri ambayo mmeionyesha kutaka kwa mara ya kwanza mnataka kwenda kubadilisha kwenda kufanya marekebisho kwenye mfumo wa grid na tayari tumeona inahitajika zaidi ya Trilioni Nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Mheshimiwa Rais ndiyo maana nimesema anaenda kufanya maamuzi magumu ya kimapinduzi tayari kwenye bajeti hii mmetenga 500 billion, that’s not small money! Niliwahi kuongea hapa lazima TANESCO muende na teknolojia kwa sababu mnapoenda kubadilisha sijui transformer kupitia hizi 500 billion, mtapoenda kubadilisha nguzo na nyaya itabidi mkate umeme ili mfanye hayo marekebisho lakini duniani ipo teknolojia ya kufanya haya na umeme uendelee kuwepo, ipo live line technology tunaomba muitumie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Dar es Salaam mnabadilisha nguzo kutoka za miti kwenda za zege inabidi mzime umeme mnapoteza mapato, wakati mnaweza mkaichukua live line mukaiweka kwenye hilo zoezi lenu mkaendelea kupata hela za umeme na mkabadilisha mifumo yenu. Kwa hiyo, naomba kwa kweli Wizara ichukulie kwa umakini sana suala la kutumia live line.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaenda kuweka transformers kupitia kwenye miradi ya REA, TANESCO kama hivi, maana yake hapa mna bajeti kuweka transformer zaidi ya 6,000, tunajua kuna baadhi ya maeneo kama kwa Babu zangu huko Usukumani, Rukwa kuna radi nyingi sana, kuna sehemu unaweza ukapoteza kwa mwaka transformer tatu, yaani transformer hiyo moja inaharibika mara tatu kuna vifa vinaitwa combi units, vile vifaa vinaenda kuzuia ile transformer isiungue kutokana na radi hii itasaidia pia kuokoa kwa sababu tayari Shirika letu lina madeni mengi. Kwa hiyo, kupunguza gharama ambazo zinaweza zikaepukika naomba pia mkaangalie hiyo teknolojia ya combi unit.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu REA ninawapongeza sana Wizara kwa sababu wote tulikuwa tushaweka kwenye mindset kwamba Rural Energy Electrification Agency kwamba ni wakala wa kupeleka umeme vijijini. Lakini mmebadilisha kwa sababu siku umeme ukishafika nchi nzima REA ife, mmeenda kusema kwamba sasa hivi ni wakala wa kupeleka nishati vijijini, that’s the way to go! Hayo ndiyo mambo ambayo tunataka kuyaona, mkimaliza kuweka umeme nchi nzima mnaenda sasa kupeleka nishati mbadala na nishati zingine kule vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimependa kuunga mkono mpango wenu wa vitongoji, kwa sababu kuna Mheshimiwa Mbunge aliwahi kusema hapa, kadri unavyozidi kutanua unazidi kutamani. Sasa umeme umefika vijijini haujafika vitongojini, kwa hiyo mpango huu wa kupeleka umeme vitongojini ni mzuri sana lakini kabla ya kuendelea nao kuna baadhi ya Waheshimiwa walishauri tuangalie yale maeneo ambayo umeme umefika lakini baadhi ya nyumba hazijapata umeme ili tunapoenda kwenye hili la vitongoji hili la vijiji liwe limekaa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri sasa nakuja kwenye jambo kubwa ambalo nina imani kwa utulivu wako, kwa akili zako, kwa uweledi wako, ukitulia kwenye mradi wa LNG unaenda kuacha historia ya kudumu katika Taifa hili, kwa kweli vizazi na vizazi vitakukumbuka, mfupa huu umeshindikana zaidi ya miaka 10 leo hii umetutolea kauli baada ya Tarehe 09 Juni tunaenda kusaini HGA kwa hiyo nikupongeze kwa hilo. Naomba uangalie sana vitu viwili, tunaye jirani yetu Msumbiji ameanza hili tumeona anavyosumbuka kwenye suala la usalama nasema kwa sauti ndogo kwa sababu tunajua, naomba tujipange vizuri neema lazima inaambatana na hofu ya usalama.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mariam Ditopile kwa mchango wako mzuri.

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti ni suala muhimu linalowezesha kupata taarifa sahihi na kuwezesha kuweka mipango mbalimbali ya nchi. Ili kupata maendeleo endelevu katika michezo, ni muhimu kuwa na taarifa sahihi zilizofanyiwa utafiti. Serikali imefanya tafiti nyingi kama vile michezo kwa watu wenye ulemavu, michezo na UKIMWI, haiba na michezo na kadhalika. Bado kuna maeneo mengi ya michezo yanahitaji kufanyiwa tafiti ili kuongeza tija katika sekta ya michezo nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo la kukosekana mfumo endelevu wa kuviendeleza vipaji vinavyoibuliwa na kuwa na miundombinu isiyokidhi mahitaji. Vilevile somo la elimu ya michezo limekuwa halifundishwi kikamilifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya mwaka 2002 hadi 2007 kulifanyika utafiti uliofanywa na Idara ya Elimu ya Michezo na Utamaduni ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ulioonyesha kwamba vipindi vya masomo ya michezo katika shule za sekondari za Serikali na binafsi vimekuwa vikitumika kufundisha masomo mengine badala ya elimu ya michezo na michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, tafiti hizi zilibainisha ukosefu wa walimu wenye sifa stahiki za kufundisha elimu ya michezo kuwa ni changamoto kwa shule za Serikali na binafsi nchini. Nashauri Mheshimiwa Waziri aanze na shule za binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokuwepo kwa mfumo na utaratibu mzuri wa ufuatiliaji na tathmini katika michezo kumeendelea kuathiri upatikanaji wa taarifa na mapato halisi yanayotokana na ajira za wanamichezo. Hali hii imeathiri wachezaji na wadau mbalimbali kuwekeza katika sekta hii ikilinganishwa na nchi kama Nigeria, Ivory Coast, Ghana na Afrika ya Kusini ambazo zimefanikiwa kupitia michezo. Mheshimiwa Waziri, hili linaendana sambamba na sanaa, hususan muziki wa kizazi kipya. Kwa mfano, Diamond ndiye msanii anayelipwa zaidi kuliko msanii yeyote Afrika Mashariki na Kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka Disemba, 2015, Tanzania ilikuwa na wachezaji takribani kumi wanaocheza michezo ya kulipwa nje ya nchi. Tisa ni wa soka na mmoja wa mpira wa kikapu. Hata hivyo, mtazamo wa jamii haujajielekeza kutambua kuwa michezo ina michango katika kukuza uchumi wa nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri Mheshimiwa Waziri, tuweze kutafuta wabia zaidi tuweze kujenga sports academy kama ile Jakaya Kikwete Sports Academy, ikiwezekana kila mkoa au angalau kila kanda kwa kuanzia.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Awali ya yote napenda kusema kwamba naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Simbachawene kwa asilimia mia moja. Pia nampongeza Mheshimiwa Rais, kwa kweli amekuwa kwa hakika akiwa ni mtekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Kwa kulifanya Dodoma kuwa Jiji, tuna uhakika sasa kweli Makao Makuu ya nchi yapo Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, narejea tena kumpongeza Mheshimiwa Rais na nimwambie, mimi kama mwakilishi wa vijana kutoka Mkoa wa Dodoma ambao sisi ndio tupo zaidi ya asilimia 60 ya population kwamba hilo tumelipokea na kwa kweli tutapokea changamoto zote na Dodoma kweli litakuwa Jiji. Niseme tu, kwa hili kumrudishia, tunajua mtanange 2020 upo, atashinda kwa asilimia kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna nchi za wenzetu hapa Afrika zimeweza. Mfano Nigeria na ya pili, South Africa. Kama wao wameweza na sisi tutaweza. Kwa hiyo, kama kuna mtu yeyote ambaye hajaunga mkono hoja hii, ajue kwamba sisi tumeweza na tutaweza. Kwa hiyo, la msingi tu apande pamoja na sisi tushirikiane kwa ajili ya kuhamisha Makao yetu Makuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, Mheshimiwa Rais alisema Morogoro kwamba katikati pazuri. Dodoma tumelala katikati ya nchi ya Tanzania na tunaona barabara imejengwa chini ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi, kuunganisha Iringa, Arusha na nchi ambazo zipo Kanda ya Ziwa. (Makofi)

Kwa hiyo, kuweka Makao Makuu hapa katikati kutarahisisha hata uchumi wa ujenzi wa viwanda na huduma zote. Mtu kutoka Arusha ili apate huduma za Kiserikali hawezi kuzunguka kwenda mpaka Dar es Salaam. Mtu kutoka Iringa, Mbeya ni rahisi kufika Dodoma kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme jamani, katikati pazuri. Kweli Mheshimiwa Rais tunamshukuru, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali (Na. 2) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza).
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwa kweli leo hii nitajikita kwenye kuongelea mchuzi wa zabibu. Kila siku nikiwa nachangia masuala ya kilimo nasema tujikite kwenye agricultural zone. Leo hii kulibeba zao la zabibu kwa Mkoa wa Dodoma, ndio mambo yenyewe tunaenda kuyatengeneza vizuri. Msimu uliopita wakulima wetu zabibu ziliozea kwenye mashamba na sababu inajulikana. Wale wenye viwanda vikubwa hapa Dodoma ambao CETAWICO pamoja na Alko Vintage yake matanki yao ya kuhifadhi michuzi yalijaa kutokana na tozo ilivyokuwa kubwa walishindwa kwenda kuuza ule mchuzi, kwa hiyo effect yake ikashuka kwa mkulima, walishindwa kuuza zabibu, zabibu zikaoza. Kwa hiyo, niseme hatua ya kupunguza punguzo kubwa sana litaenda kuwahakikishia soko la zabibu za wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waswahili wanasema usione vinaelea vimeundwa. kwa namna ya kipekee nikupongeze umekuwa pioneer kwenye kutetea punguzo hili; mbele ya Waziri Mkuu na Rais uliongea. Mwingine pia Mbunge wangu wa Dodoma Mjini Mheshimiwa Anthony Peter Mavunde ambaye anajinasibu kwa kusema yeye ni mtumishi wa watu (De populo servorum) sijui kama nimepatia Kigogo hiki. Mbele ya Rais tarehe 3 Novemba, wakati wa ufunguzi wa NMB aliomba hili punguzo mbele ya Waziri Mkuu na Mbele ya Makamu wa Rais aliomba hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna siku nimeambatana naye mpaka Ofisi za TRA akitetea punguzo hili, hawezi kujisemea humu ndani lakini naomba niwahakikishie wakulima wote wa Dodoma Mjini kwenye hili Mbunge wenu amelipigania na fadhila mumrudishe 2020 kijana wenu, aliwasemea na kweli amehakikisha yeye ni mtumishi wenu. Atapita bila kupingwa, hilo linajulikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nasema mbona tunaanza kusutana? Wameongea wamesikika, mambo yamerekebishika wanaanza tena kusuta ooh! Mheshimiwa Dkt. Mpango hasikii, amesikia. Asingerekibisha wangesema nini? Kwa hiyo, ifike hatua kama kweli tunashauri ili mambo yawe vizuri, basi tusifie tuendelee kuongezea nyama sio tunaanza tena kusutana sutana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, napenda pale pale uliposema wewe kuhusu hii import permit. Jamani hata kwenye suala la uchenjuaji walivyosema kwamba kama kuchenjua kufanyike kwenye mkoa ule ule ambao, tumeona effect yake. Kulikuwa wanaoleta madini yao kutoka Congo na Kenya kuja kuchenjua, tumekosa mapato kutokana na hilo. Kama leo vijana wetu wanapata uwezo wanaenda huko Mozambique na wapi kuchukua madini kuja ku-process hapa kwa nini tuanze kuleta vikwazo? Kwa kweli kwenye hili Mheshimiwa Waziri wa Fedha kama vile tunavyom-appreciate yeye ni msikivu na mwelewa, hebu aangalie namna ya kuliweka sawa. Yote haya tunataka vijana wetu wapate ajira na vilevile nchi yetu iweze kupata mapato kama wanavyofanya Awamu ya Tano wanajenga vituo vya afya, tunaona kodi, hata TRA acheni wachukue kodi ya majengo, wananchi wanaona namna Serikali ya Awamu ya Tano inavyorudi kwao na mapato yanatumika vizuri na kwa uwazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia katika hoja zilizo mbele yetu. Kwa vile ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge hili Tukufu, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema, kwa kuniwezesha kuwa mwakilishi wa vijana katika Bunge hili Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite moja kwa moja kwenye mchango wangu. Naanza na asilimia tano ya mikopo kwa vijana kutoka kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri zetu. Naomba kuishauri Serikali kwamba hili jambo ni la kutilia mkazo maana limekuwa kama ngonjera. Kila siku watu wanaongelea kwamba kuna 10% Halmashauri zinatakiwa zitoe 5% iende kwenye vikundi vya akinamama na 5% ziende kwenye vikundi vya vijana lakini haifanyiki hivyo.
Mheshimiwa Spika, sasa kwa Serikali hii ya Awamu ya Tano na kasi yake iliyoanza nayo kwa ajili ya kuwatumikia wananchi basi tunasema na hawa watu wa Halmashauri wajue kwamba huu ni wajibu, ni lazima watoe hizi fedha. Pia siyo kutoa tu zipangiwe utaratibu maana hii ni mikopo, lengo lake ni kwenda kuwasaidia hawa vijana waweze kufanya kazi, waweze kuinua kipato chao na vilevile hizi pesa zirudi ili vijana wengine wapate hiyo fursa. Kwa hiyo, uwekwe utaratibu mzuri wa kuzikopesha na kuzirudisha ili ziwe endelevu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri awaambie Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya walisimamie kwa karibu jambo hili. Huu ni mpango wa Serikali lakini tumeona kuna vyama vingine vya siasa sijui wanalewa madaraka, juzi tu wameanza kutoa hundi, ooh, mapesa ya UKAWA, mapesa ya UKAWA ya wapi? Basi na sisi wa CCM kwenye Halmashauri tunazoziongoza tuanze kusema ni hela za CCM. Kwa hiyo, naomba ifahamike kwa wananchi kwamba huu ni mpango wa Serikali na siyo mpango wa vyama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye elimu. Napenda kuipongeza Serikali hii, tangu tulipokuwa tunaomba ridhaa kwa wananchi tulisema kwamba tuko kwa ajili ya kuwasaidia wananchi. Mmethubutu na mmeweza kuleta elimu msingi bila ya malipo, kazeni buti mwende mbele. Kitu chochote chenye neema lazima kiendane na changamoto. Tumeona udahili umeongezeka baada ya kuwawezesha wananchi kwani ile Sh. 20,000/= tu ya kumpeleka mtoto wake shule ilikuwa inamshinda.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kutokana na neema hii kuna vitu vimeambatana nayo, kuna upungufu wa madarasa, Walimu, matundu ya vyoo halikadhalika na kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya hawa Walimu wetu. Nashauri katika kila Halmashauri waweke mpango mzuri wa kuweza kutatua matatizo ambayo yanaambatana na neema hii bila kusahau madawati. Pia niwakumbushe tu ameshaongea Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba kila Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi zile mbao mlizozikamata jamani ziende zikatengeneze madawati, ameongea bosi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niongelee kuhusu sekta ya afya katika upatikanaji vifaa tiba na dawa. Hii imekuwa changamoto ambayo najua Serikali inajaribu kuikabili kutwa kucha. Tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, tukaeni chini tuna wataalam, Wizara yetu ya TAMISEMI ikishirikiana na Wizara ya Afya, Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na Wizara ya Viwanda na Biashara kwani hatuwezi sisi kama Tanzania kuwa na viwanda ambavyo vitatengeneza dawa? Nina uhakika malighafi za kutengenezea dawa zipo.
Mheshimiwa Spika, Watani zangu Wahaya mtu akiumwa kichwa hanywi panadol ana dawa zake anazitumia. Nina uhakika malighafi za kutengeneza dawa tunazo, hiyo itatuokoa kwanza tutakuwa tunazalisha dawa zetu hapa, tutapata kipato soko lipo na pia dawa zitakuwa zinapatikana kwa bei nafuu na tutawaepuka hawa matapeli ambao wanatafuta fursa ya kuleta dawa ambazo zimepitwa na muda na siyo nzuri kwa matumizi ya binadamu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuzungumzia mradi wa uendelezaji miji ya kimkakati. Kwa Mkoa wetu wa Dodoma huu mradi umetusaidia sana kwenye maeneo ya Kisasa, Nkuhungu, Mjini Kati na Kikuyu. Kwa kweli mradi huu ulivyotekelezwa hapa mmetupa moyo, kweli mnatuheshimu kwamba hapa ni Makao Makuu ya Chama na Serikali. Kwa hiyo, naomba mradi huu uendelee kwenye sekta zingine za miundombinu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kugusia Tume ya Utumishi wa Walimu. Hiki kimekuwa ni kilio kikubwa sana kwa Walimu wetu. Tunajua mchango wao katika maendeleo ya Taifa letu kwa sababu aliyekuwa anaajiri Mwalimu ni mwingine, aliyekuwa anashughulika na kuwalipa Walimu ni mwingine, aliyekuwa anashughulika na kumpandisha cheo Mwalimu ni mwingine, aliyekuwa anashughulika na malipo ya Mwalimu ni mwingine, lakini Tume hii ya Utumishi itakuja kuwa mkombozi wa Mwalimu, hongera sana kwa Serikali yetu. Kwenye bajeti hii tumeona mmeshawawekea fungu lakini tunaomba kwa siku za karibuni muweze kukamilisha taratibu zote ili hii Tume ipewe meno ianze kazi haraka sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nigusie kidogo mipango ya matumizi bora ya ardhi. Wataalam wetu katika Halmashauri wakishirikiana na Viongozi wa Vijiji, Kata, pamoja na Wilaya na Madiwani wapange mipango bora ya ardhi kwa sababu huko ndiko kwenye wananchi na wanajua changamoto zinazotokea na ambazo zinaleta ugomvi kati ya wakulima na wafugaji. Tukikazania huko hili tatizo litakuwa historia kwa sababu wananchi wanaumia jamani. Sisi tupo huku lakini wananchi wa Kongwa tunaumia sana kwa hii migogoro ya ardhi baina ya wakulima na wafugaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia napenda tu kugusia kwa hawa watumishi wa Halmashauri, kuna hawa Mabwana Kilimo, Mabwana Mifugo na Maafisa Biashara, majipu tusiangalie wale wanaofuja pesa tu tuwaangalie hata wale watumishi ambao hawatoi deliverance. Wananchi wetu wanajitahidi kujikwamua kwa kuendesha shughuli za kilimo na biashara lakini hawa wataalam hawawasaidii. Vijana wengi wapo hapa Dodoma wanafanya biashara ya uchuuzi wa mazao lakini hakuna Afisa Biashara hata siku moja kamfuata kumpa ushauri wa kitaalam. Vilevile Serikali ifike kipindi iwasaidie na kuwa-guarantee hawa vijana waweze kupata mikopo na wakopesheke. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuongelea makusanyo ya mapato. Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshaongea, Halmashauri wasipofikisha 80% ya ukusanyaji wa mapato waliokadiriwa zitafutwa. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu hii kauli iwe ni ya kweli, kama Halmashauri haijafika hicho kiwango basi ifutwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kugusia kwa juu tu kuhusu TASAF III, TASAF inasaidia sana. Tumeona TASAF I, TASAF II na sasa hivi tupo kwenye TASAF III ni kweli inasaidia wananchi wenye kipato cha chini na kaya maskini. Tunaomba TASAF iendelee na moyo huohuo, kelele nyingi na matatizo tuliyokutana nayo huko ni ya kisiasa kwa sababu wenzetu walisema, ooh, hizi hela zinakuja kwa ajili ya kampeni, siyo kweli, zinasaidia wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuongelea PCCB, tumeona utendaji kazi wao mzuri, wanashughulikia masuala ya rushwa lakini kwenye ripoti zao tumeona wakiongelea, ooh, tume-save fedha kiasi fulani lakini kuna rushwa fulani sijui kwa nini inafichwa. Rushwa hii inaumiza kweli kweli, inawaathiri watu kisaikolojia, inasababisha watu wapate magonjwa, wengine hata wakate tamaa za maisha, ni section 25, rushwa ya ngono hasa kwa mtoto wa kike.
Mheshimiwa Spika, mtoto wa kike tangu elimu ya msingi anasumbuliwa na rushwa ya ngono, kwenye elimu ya sekondari anasumbuliwa na rushwa ya ngono, akija chuo kikuu anasumbuliwa na rushwa hii ya ngono, akija kwenye kazi anasumbuliwa na rushwa ya ngono. Jamani kama kesi zipo tunaomba zielezwe ili hawa mabinti wasifiche na waseme haya matatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia mbili.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Naomba nitangulize shukrani zangu kwa Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na kuweza kusimama hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumpongeza Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kutimiza ahadi yake. Alisema kipindi cha kampeni, yeye akiahidi anatekeleza. Kwa Wana-Dodoma ametuletea Makao Makuu na kweli Serikali imeshahamia. Kipindi cha kampeni wananchi waliilalamikia CDA kwamba amethubutu, ameivunja mamlaka ya ustawishaji. Sisi tunamwambia tuko naye bega kwa bega, tunasema uungwana ni vitendo asubirie 2020, Dodoma tuko naye pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyongeza tu ni kwamba Serikali tunaomba sasa muda muafaka umefika wa kuleta muswada wa Sheria ya Makao Makuu. Leo hii tunajadili Wizara nyeti, tunajadili maisha robo tatu ya Watanzania. Kwa mujibu wa hotuba yako Mheshimiwa Waziri, umesema kwamba sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi, imeajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania.

Waheshimiwa Wabunge, everybody is entitled to his/ her opinion, lakini lazima tuseme ukweli. Wao wanaosema tumeganda wakati Sudan inategemea chakula kutoka Tanzania, Kenya wanategemea mahindi kutoka Tanzania, Uganda wanategemea mahindi kutoka Tanzania na mazao mengine! India wanategemea chorosho, choroko, dengu, mbaazi zote zinatoka Tanzania. La msingi ni kwamba tunatakiwa tuishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii naomba niwaambie, Waziri wa Fedha na Naibu Waziri, naomba mnisikilize. Mipango yenu ni kwamba tunataka kupeleka nchi kwenye uchumi wa viwanda, tunataka kuwa na uchumi wa kati, tuwekeze kwenye kilimo, mifugo na uvuvi. Kilimo, mifugo na uvuvi ni afya, kilimo, mifugo na uvuvi ni ajira, itampunguzia kaka yangu Antony Mavunde adha aliyokuwa nayo. Kilimo, mifugo na uvuvi ni fedha na uchumi, kilimo, mifugo na uvuvi ni amani. Tukiwa na njaa tutaweza kuwa na amani?

Kwa hiyo, Waziri wa Fedha na Mipango, ukipeleka hela kwenye kilimo, mambo yako yote, mpango wa maendeleo utafanikiwa kwa asilimia 200. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi, lawama nyingi sana zimemwendea Mheshimiwa Waziri. Namfahamu Mheshimiwa Waziri. Nimeshalima naye, ni mkulima mzuri sana. Tena bahati nzuri analimia hapa hapa katika Mkoa wetu wa Dodoma. Mheshimiwa Waziri amekua kama mtoto wa mfugaji, kazaliwa kwenye jamii ya ufugaji, anatoka Kanda ya Ziwa, anaelewa uvuvi. Ukikaa na Mheshimiwa Waziri, maono aliyokuwanayo kwa Wizara yake ni makubwa, lakini hana fedha, atafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nieleze umuhimu wa utafiti, sayansi na teknolojia katika kilimo. Kwa Kiingereza tunasema, science and technology innovation in agriculture. Tunasikitika, bajeti ya ugani iko wapi? Bajeti ya utafiti ikoje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma kitabu chote, leo hii nchi yetu ina watu takriban milioni 50, baada ya miaka 10 tutakuwa na watu zaidi ya milioni 65. Hakuna mpango mkakati wa kutuvusha kutupeleka huko na yote Mheshimiwa Waziri siyo kosa lake; huna utafiti, uta-project vipi? Utapangaje mipango yako vizuri kama hujafanya utafiti?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote, niwaambieni, dunia nzima kati ya watafiti wanaoheshimika ni Tanzania. Kigoma Watanzania walifanya utafiti wa mbegu ya michikichi ambayo Malyasia ndio wanatumia. Leo hii niwaambieni, kuna Mtanzania mmoja alikuwa Serikalini, amefyatuliwa risasi juu, amechukuliwa na Bill Gates Foundation Marekani kama mtafiti na aliombwa abaki kule afundishe masomo ya kilimo, lakini amechukua uzalendo wake, amerudi Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa utafiti naomba niwaambieni Serikali, leo hii mjiulize kwenye uvuvi, Ziwa Victoria sisi ndio wenye sehemu kubwa, lakini ukienda kwenye statistics za dunia, Uganda imetupita, yenyewe ni ya sita katika uvuvi wa Ziwa Victoria. Sisi ni wa nane, kwa nini? Leo hii tujiulize Bukoba kahawa mwaka 1978, miaka 30 na kitu iliyopita walikuwa wanazalisha zaidi ya tani 140,000, lakini leo kwenye kitabu mmeona, tuna-project kuvuna tani 47,000 kwa sababu hatujafanya tafiti ya kuendeleza hizi kahawa. Miche imekuwa mikuu, haizalishi, imekuwa dormant. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tu niwaeleze umuhimu wa science and technology innovation. Leo hii tunafurahi hapa kusema kwamba tunalisha East and Central Africa, lakini tusipojipanga vizuri, tunu hii tuliyopewa na Mwenyezi Mungu tutaikosa, Malawi wamejipanga kwenye pamba. Malawi ni nchi ndogo, lakini leo hii inaenda kutupita kwenye uzalishaji wa pamba kwa sababu ya tafiti na kujipanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuongelea suala la mbegu. Tumejaribu sana kuendeleza kilimo. Nashukuru Serikali ilijaribu kutoa matrekta, lakini hebu tuweke azimio, Mheshimiwa Waziri, kaa chini. Vituo unavyo, mahitaji unayajua, sitaki kuzungumzia sana yaliyokuwemo humu. Hebu tusonge mbele, tuwafunge watu midogo. Tuweke azimio kwamba Serikali ihakikishe kila mkulima anapata mbegu bora. Wakulima wetu wamekuwa wanatumia nafaka. Nendeni mkasome muone tofauti ya mbegu na nafaka (seed and grain). Mkulima analima heka yake moja, akivuna mahindi, yale yale aliyoyavuna, anahifadhi anaifanya mbegu. Siyo mbegu! Atajikuta alivuna mawili atabaki na moja. Kwa hiyo, tuweke azimio, uwezo huo tunao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, naomba kuzungumzia Mkoa wangu wa Dodoma. Mkoa wa Dodoma unafanya tremendous kwenye kilimo, ingawa watu wanajua kwamba ni kame. Msimu wa mwaka 2013/2014 Tanzania iliuza tani 860,000 China, kati ya hizo tani 300,000 ufuta umetokea hapa Dodoma. Tuna maonyesho ya Nane Nane. Pale inaonekana mazao yote yanawezekana. Kwani ile ardhi ya Nane Nane ni ya wapi? Ni Arusha? Siyo ya Dodoma! Lakini humu sijaona Mheshimiwa Waziri. Nina vijana wengi na kila siku nawapigia kelele waingie kwenye kilimo. Hebu tuhamishe basi ile Nane Nane tuipeleke Chamwino, tuipeleke Kondoa, tuipeleke Chubi. (Makofi)

Mheshimiwa Ally Saleh kauliza kuhusu shamba kubwa, twende Chubi kwa Mheshimiwa Kijaji ukaone shamba kubwa za hizo heka unazosema na mwekezaji ujifunze. Tembea, no research, no right to speak. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naongea kwa sababu niko field, najua raha ya kilimo, najua machungu ya kilimo, najua mafanikio na ninajua tukiweka nguvu kidogo, tutafika mbali. Nataka sana vijana. Vijana wanataka red market, wanataka mitaji, hatuna sehemu ya kuwapeleka zaidi ya kilimo. Tuwekeze jamani! Leo hii haiwezekani, nchi ya Egypt ina River Nile peke yake. Source ya River Nile ni Lake Victoria. Kale ka-Nile kanatokana na Lake Victoria wanakatumia, wanafanikiwa vibaya mno! Sisi wenye Ziwa Victoria, wenye Ruvu na mito kibao hatuongei, kwa nini tunashindwa kutumia hizi fursa? Tumeona mwenyewe Mheshimiwa Waziri umeshasema hii ndiyo sekta ambayo inaleta pesa kuliko zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nigusie kwenye uvuvi katika Ziwa Victoria, kuna samaki anaitwa sangara. Sangara jamani…(Makofi)

(Hapa kengele ililie kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kutoa mchango wangu. Natangulia kwa kusema kauli inayosema nitasema ukweli daima fitina kwangu mwiko. Naenda kuchangia ukweli siyo fitina wala majungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, napenda kuwapongeza viongozi wetu wakuu wawili: Rais wa nchi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Waziri Mkuu, wameonekana namna gani wana dhamira ya dhati kuwasaidia Watanzania. Katika ziara zake zote Mheshimiwa Rais lazima atatue matatizo ya wakulima, hata Waziri Mkuu tumeona akihangaika kwenye kahawa, korosho, tumbaku kwa kweli hawa viongozi wetu kwenye hili wanapaswa kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Dkt. Tizeba ni swahiba wangu lakini leo naomba nimwambie uswahiba baina yangu mimi na yeye haujazidi uswahiba niliokuwa nao na wakulima wa nchi hii. Najua jasho wanalolitoa, najua jinsi gani wanavyojikwamua na mazingira magumu lakini wanataka kupatia uchumi wetu kipato kikubwa. Kwa hiyo, leo hii nasimama kwa niaba ya wakulima wangu wa Chubi, Chamwino, Dodoma Mjini, Kondoa, Chemba, Soya, kote naomba niongelee machungu yanayowapata na naongea kwa facts. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na zao la mahindi. Tanzania ilishatoka kwenye kilimo cha subsistence, hatulimi mahindi kwa ajili ya chakula, tunalima mahindi kwa ajili ya biashara na chakula. Leo hii ripoti yake yeye mwenyewe inamsuta amesema tumezalisha zaidi ya asilimia 120, kwa hiyo, suala la yeye kulinda food security asiende kuwaumiza watu ambao tunawaambia walime kwa ajili ya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe ni kijana ambaye ni mkulima, nina mwaka wa saba kwenye kilimo lakini I regret to say ni mwaka wa kwanza sijalima. Nina gunia 6,500 juzi nimetoka kuzitupa zimeoza, tunaelekea wapi? It is very simple, Mheshimiwa Tizeba anakwenda kushauri viongozi wetu wakuu anawalisha matangopori kwa nini? Leo hii tayari tuna ziada na kiada ya mahindi anaenda kuweka zuio la ku-export mahindi lakini anaruhusu mahindi yaingie basi si angeacha tuminyane wenyewe ndani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkulima hajaomba mbegu hasa sisi wa Kanda ya Kati, Dodoma tunalima katika hali ngumu, anasema ili kwa Mheshimiwa Musukuma wasife njaa atuumize sisi. Musukuma ana madini, ana ziwa kule anavua samaki, sisi tunategemea kilimo, kilimo chenyewe ni cha machungu kweli kweli hatupati lolote kutoka Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii mahindi yameoza hali ni mbaya, anajibu majibu kirahisi oh hao wachuuzi, kwani wachuuzi wanaenda kununua na mawe yale mahindi? Mkulima kitu chochote akishavuna, amekaa miezi saba anasubiria kitu chini ya ardhi hajui hatma yake, anavuna mahindi yeye anachotaka apate hela aendelee na maisha, alipie watoto ada, aweze kula, aweze kujitibu anasema simply wachuuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mkiwasema wachuuzi ndiyo vijana wangu wengi wa hapa Dodoma wamejiajiri katika sekta hiyo na hawa ndiyo wa kuwasaidia. Hebu tutathmini leo hii exporters wangapi wana asili ya Kitanzania? Sasa kama hatutowashika hawa mkono kuwapandisha tutazidi tu kuwa na wale wageni ambao ndiyo wanapeleka mazao nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni-regret sana kwenye mahindi kwa kweli basi angalau ungesema tunakataza kutoa nje lakini tusiingize kutoka nje ya nchi. Leo hii Zambia wameingiza mahindi mengi Mtwara, Lindi mpaka Himo, mahindi yetu yamekwama hakuna soko, huo ndio ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye tumbaku, kwa sababu anajitetea sana Mheshimiwa Waziri. Uongozi una vitu viwili, sawa bajeti anapelekewa ndogo lakini kuna utashi, Waziri ana utashi gani, hapa umesoma hotuba yako hata hatujasisimkwa sisi kama wakulima. Bajeti ya kwanza aliongea Mheshimiwa Mwigulu hapa kila mtu alisisimka kama mkulima alisema kabisa sasa hivi yale mageti hakuna kuzuia magunia ya wakulima muwaache. Alienda kutatua kero ambayo inamgusa mkulima wa kawaida, but now nothing my friend, nothing. Sawa Waziri anapelekewa bajeti ndogo lakini utashi, ameaminiwa na Mheshimiwa Rais apeleke kilimo kwa ajili ya kuleta uchumi wa viwanda lakini ndiye yeye anavuruga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, world market price ya tumbaku, Cost, Insurance and Freight mpaka Vietnam ilikuwa kilo moja ni dola 2.20. Wanunuzi wetu hapa walikuwa tayari kwa sababu ununuzi wa tumbaku ni pre-order, walikuwa tayari kununua zaidi ya order waliyotaka lakini wakaomba wanunue kwa dola 1.3 lakini Mheshimiwa Waziri akakataa huku akijinadi kwamba ana wanunuzi. Akaenda nasema tena tangopori akamlisha Mkuu, akamlisha Mheshimiwa Waziri Mkuu lakini Wabunge wa Tabora huku walichachamaa wakasema mbona wanunuzi wanazuiwa kununua na tumbaku zinakaa muda mrefu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbe inavyosemekana Waziri alisema kwamba wanataka kununua kwenye 0.8 lakini ilikuwa wanataka kununua kwa 1.3. Kilichotokea mvua imenyesha, hawana vihenge wale, hawana sehemu ya kuhifadhia, wanalima ili wauze waweze kuendelea na maisha mengine, tumbaku zimeharibika, zimeshuka thamani, mwisho wa siku wameuza kwa 0.8 USD. Kwa hiyo, zile pesa walizopata wameenda kulipa tu madeni hakuna chochote yaani kwa kweli wenzangu Wabunge wa Tabora watakuja kusema hali halisi, mimi ni Mbunge wa nchi nzima kwa hiyo lazima niliongelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye korosho. Picha tunayoipata kwenye korosho kwa kweli niwaambieni siyo juhudi za Wizara, ni kudra ya Mwenyezi Mungu. Tuna advantage kwamba msimu unapoanza sisi ndiyo nchi ya kwanza ya kuvuna korosho, kwa hiyo, tunakuta makampuni mengi yanahitaji ile korosho. Ndiyo maana mpaka leo korosho ina bei ya juu tunapoona kwenye minada. Vilevile in the world Tandahimba, Newala, Masasi na Mtwara ndiyo ambao wana-produce korosho nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, I was in India, nilienda kuongea na watu kwa ajili ya kuwauzia korosho bahati mbaya niliharibu kwa sababu nilikuwa na rafiki yangu kutoka Ghana, wale waliniambia Ghana nao wana korosho nzuri but still virgin hawajagundua, basi maneno yale hayajaenda kushoto wala kulia, Ghana wamezindua Mpango wa Miaka Kumi wa Kunyanyua Kilimo cha Korosho, tusubiri tutakayoona, hatuna mipango endelevu. Bodi ya Korosho wanai-disturb, korosho ni zao la biashara, linaenda vizuri, linaleta mapato, ghafla unasema sulphur ipelekwe bure waliomba, ndiyo mahitaji ya wakulima? Mmeshindwa kuzifikisha kwa wakati korosho zikaingia magonjwa hakuna dawa ya kutibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, magunia, minada imeanza, mtu ana korosho zake nyumbani hamna magunia na yaliyomo chini naomba vyombo vya ulinzi na usalama vikachunguze mnajua wenyewe. Haya leo hii wamerudi tena nyuma, kwa nini tuna-disturb industry? Wamerudi nyuma tena wanasema ooh sulphur hatuzitoi bure, mliombwa mtoe bure? Kwa nini mna-disturb wakulima na watu wanaenda katika njia nzuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mipango endelevu tuliyokuwa nayo leo hii badala ya kutoa korosho kama raw material tunaenda kuongeza miche. Mimi napenda kwamba kila sehemu tulime korosho kwa sababu it is a green gold lakini nilitoa hapa mchango mwaka wa kwanza nikasema tuweke agricultural zone, kila sehemu hapa ina zao lake, kwa nini tusikazanie huko? Unaniletea mikorosho Dodoma hakuna hata Afisa Kilimo mmoja aliyefundishwa utaalamu, hiyo mikorosho ikiota asilimia 10 najiuzulu Ubunge, iko majumbani imekauka. Unawapelekea watu hujawapa utaalam, tena system unayo, kuna Maafisa Ugani kila Kata na Kijiji, waite wape elimu halafu ndiyo usambaze, hamtoi elimu mnaenda kugawa mikorosho, tutaona mwisho wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu mimi niwashauri kidogo tu, tuweke mazingira mazuri, huwezi ukampa mazingira sawa mtu anaye-process korosho na yule anayeitoa nje, hebu tuwa-favor hawa. Kuna kitu kinaitwa opportunity cost ingieni.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia kwenye taarifa ya Kamati hizi mbili. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu aliotujalia afya na uzima kuweza kukaa kwenye kikao hiki leo.

Mheshimiwa Spika, mimi ni mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini lakini pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati. Kwa hiyo nipende kumshukuru sana na kumpongeza Mwenyekiti wetu wa Kamati Mheshimiwa Kitandula kwa uongozi wake mahiri na kutuongoza vema. Tunamuombea afya na uzima ili aendelee katika majukumu yake. Pia nipende kuwashukuru sana wajumbe wa kamati hasa wale wanashiriki katika vikao na ziara kikamilifu; lakini pia niwatie joto wale ambao wanategatega katika kazi za kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kamati yetu inafanya kazi na wizara mbili, Wizara ya Nishati pamoja na Wizara ya Madini, nipende kuwapongeza sana sana Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara hizi pamoja na Manaibu wake, pamoja na Makatibu Wakuu lakini bila kuwasahau wataalam wa wizara hizo. Kwa kweli wanafanya kazi kubwa katika kutafsiri maono ya Mheshimiwa Rais ya kuleta uchumi wa kati na Tanzania ya viwanda. Pia kubwa lile la kutaka sisi kujitegemea kama taifa huru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sekta ya nishati, nirudie kuunga mkono kauli ya mchangiaji aliyepita Mheshimiwa Peter Serukamba ambaye amesema kwa uthubutu wa Viongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano kweli yanafanyika mapinduzi makubwa na ya kihistoria. Kwenye sekta ya nishati leo hii mtu anavyosema kwamba tuna umeme wa ziada, ndivyo taifa linatakiwa liwe kwa sababu ulichonacho na huku una mipango endelevu lazima uwe na ziada na uwe na mipango ya kuongeza zaidi na zaidi. Huwezi kusema ninahitaji thelathini na nina hiyo hiyo thelathini halafu ukasema wewe ni taifa linaloendelea. Kwa hiyo tunapoongea kwa sababu wamesema ooh, wateja ni hawa tu na huku tuna umeme wa ziada. Taifa lolote lenye mipango endelevu na ambalo liko katika process ya maendeleo lazima liwe na ziada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona mafanikio makubwa ya miradi hii ya umeme vijijini, awamu ya kwanza, awamu ya pili na sasa tuko kwenye awamu ya tatu ambayo ina mafanikio makubwa. Ilipanga kupeleka umeme kwenye vijiji 4,651; miezi 19 ya utekelezaji tayari vijiji 3,269 vimeshafikiwa na umeme ambayo ni sawa na asilimia 70 ya malengo waliyojiwekea. Wilaya ya Tarime ambayo ina majimbo mawili ina vijiji 88, kwenye vijiji 88 tayari vijiji zaidi ya 46 vina umeme, vijiji zaidi ya 26 vimeshaingia kwenye bajeti ya mwaka huu kazi zinaendelea kusimamisha nguzo na nyaya ili umeme uwake kwenye vijiji hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika nchi za Afrika ni takribani mataifa kama manne tu ikiwemo Nigeria ambao wanafanya process hii ya ku- electrify rural areas. Lakini kati ya yote sisi Tanzania tuko bora hata Angola wamekuja nyuma yetu wamekuja kujifunza Tanzania kufanya electrification kwenye vijiji vyao, kwa hiyo kazi inafanyika na sio kazi ndogo ni kazi kubwa kweli kweli.

Mheshimiwa Spika, zipo changamoto lakini uzuri wa viongozi wetu ni wasikivu. Tuliwaambia wigo (scope) ni mdogo ndio maana Wizara kupitia REA wakasema tulete awamu ya tatu mzunguko wa pili ili kufanya ujazilizi kwenye maeneo ambayo yamerukwarukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo changamoto za vifaa kwamba hawa wakandarasi wanakuwa kidogo wana uzito katika kutekeleza majukumu na visingizio kwamba hawapati vifaa, lakini nashukuru kwa ushauri wa Kamati Serikali tumesikia juzi walikuwa na mkutano na wakandarasi kwa maana sasa wanachukua maoni yetu na kuyafanyia kazi. Bunge kazi yake ni kuisimamia na kuishauri Serikali, ukiacha kupitisha bajeti. Mafanikio mema ya Serikali ndio mafanikio yetu sisi Bunge. Sasa leo hii ukisimama kama Mbunge na kubeza mafanikio ya Serikali labda kwa vile ndio uki upande wa kukataa, lakini ukweli upo na unaonekana.

Mheshimiwa Spika, Shirika la TANESCO ni shirika la umma. Serikali hii ilipoingia madarakani Awamu ya Tano TANESCO ilikuwa ni shirika la madeni na shirika ambalo lilikuwa linaendeshwa kwa kupokea ruzuku kutoka Serikalini. Lakini leo tunavyoongea TANESCO inalipa madeni, TANESCO haipokei ruzuku, TANESCO haizalishi madeni, TANESCO inasonga mbele. Tunasema mapinduzi makubwa leo hii tuna ziada ya umeme, lakini bado Serikali hii kwa kutumia fedha za ndani ambazo Bunge hili ndio limeidhinisha tuna ujenzi wa umeme kwenye Bwawa la Rufiji la Nyerere. Kwa hiyo kwa kweli mambo ni makubwa na sisi kama Kamati/Wajumbe tuwatie moyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye sekta ya madini kwa kupitia sheria zile mbili za mwaka 2017 lakini pia mabadiliko ya sheria ndogo ya mwaka 2019 tujivunie, Tanzania leo hii madini ni mali ya Watanzania. Leo kuna masoko ya madini, leo kuna kipengele kwa kuanzisha Tume ya Madini, kuna kitu kinaitwa local content. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka mayai, kabichi yalikuwa yanaingizwa kutoka nje ya nchi, leo mama wa kawaida pale nyumbani kwa Mheshimiwa Spika anauza mayai mgodini. Sasa kama hatutofurahi kuona kwamba haya manufaa yanashuka kwa wananchi wa chini tunalipenda Taifa letu, utabeza mambo yote haya ambayo yanamgusa mpaka Mtanzania wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii kule Geita inajenga refinery ambayo itaenda kutalisha haijawahi kutokea kwenye historia ya nchi. Kwanza hiyo refinery Afrika Mashariki ndio itakuwa ambayo ni modern kuliko zote, itaweza ku-process zaidi ya tani 100 ya dhahabu kwa mwaka. Dhahabu yote inayozalishwa Kanda ya Ziwa itakuwa inapandishwa thamani pale. Mambo ni makubwa nan i mengi lakini tumeona mapato, Mheshimiwa Rais alisema hatutaki sisi ndio haya mambo sasa hivi tunapiga watu wa Marekani. Wewe Marekani umemzuia sisi Mkuu wa Mkoa wetu ni mtu mkubwa, yule ni president appointee, sasa leo unamzuia asiingie nchini kwako na sisi tusijibu kisa wanatupa hela za msaada ndio maana tunataka kujitegemea ili mtu anapotoa kisu na sisi tunatoa panga msichukue tafsiri nyingine nimetumia mfano maana kwa kunani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tuna shirika la Twiga Mining Company hayo siyo mafanikio? Kweli hatuendi kwenye uchumi wa kati. Leo hii Tanzanite kwa ujenzi wa ukuta ilikuwa inapatikana Tanzanite kilo 147.7 leo tunapata kilo 949; mapato kwenye madini yametoka kutoka bilioni 196 mwaka 2016 mpaka bilioni 310 inachangia katika pato la Taifa utasema mambo hayajafanyika! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huwezi kujua umuhimu wa hivi vitu kama hujatoka nje ya mipaka ya Tanzania. Ulinipa heshima kwenda kushiriki round table ya viongozi wa nchi wa SADC kwenda kutoa maoni namna gani ya kubadilisha policies na sheria ili kuboresha extractive industry iweze kutufaidisha sisi kama wazawa, kila nchi ilikuwa ina-present mawazo, Tanzania tulikuwa ni nchi mfano, a model country. Walisubiri sisi tuwasilishe ili wao waweze kupata dondoo. Nakushukuru na ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Ninukuu maneno ya Mheshimiwa Rais wetu Kipenzi Mama Samia Suluhu Hassan aliyozungumza pale Dodoma UDOM akiwa anaongea na viongozi wa dini mbalimbali. Alisema, Wabunge tulieni, acheni kudemka. Sasa sijui hatukumwelewa! Kwa sababu leo hii wananchi wetu wana changamoto nyingi, wanatutaka sisi Wabunge wao tuje hapa tuielekeze na kuieleza Serikali namna gani ya kuunga mkono juhudi za Rais wetu ili Tanzania ifike kwenye nchi ya ahadi. Leo hii tunapoteza masaa yote kwa ajili yao kudemka na kutafuta kiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kaka yangu Bishop Gwajima anajua ni namna gani ninampenda na tunaongea mambo mengi, lakini mimi siyo mnafiki. Nilimwandikia ujumbe mfupi kwenye WhatsApp nikamwambia kaka hapa umepotoka. Hatukatai kutokukubali chanjo; na ndiyo maana msimamo wa Serikali chanjo ni hiari, lakini mwenzetu huyu anatumia vibaya kanisa lake kwenda kuweka tuhuma nzito kwa viongozi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unaposema viongozi wamepewa fedha, Mheshimiwa Rais amepokea rushwa, ndicho unachomaanisha. Ukisema viongozi wetu chanjo wanazopigwa wanadanganya, unamaanisha Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Spika ambaye kwa kweli ndio anayetuongoza hapa, Waziri Mkuu na wote waliochanja wanawadanganya Watanzania. Ni vizuri mmemwita mbele ya Kamati ameshindwa kuleta vielelezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kawe kwenye chama chetu waligombea wengi. Kawe kwenye Uchaguzi Mkuu viligombea vyama vingi na alitupa mzigo mkubwa sana. Ilibidi twende Roman Catholic tufute mambo aliyoyasema, ilibidi twende kwa Waislamu tufute mambo aliyoyasema, chama kimemwamini, wananchi wa Kawe wamemwamini, ana majukumu ya kuwatumikia wananchi wa Kawe, arudi kwenye mstari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kaka yangu Mheshimiwa Jerry Silaa kwanza sisi kama vijana wenzake; sijui wasomi wenzake wanasheria, maana mimi sio penguin; tumesikitishwa mno na drama zako. Umeitwa kwenye Kamati, jishushe brother, tuna safari ndefu. Unamtunishia misuli Ndugai, mwenzako kawa Mwenyekiti, Naibu Spika, Spika miaka kumi. Kongwa mimi mwekezaji kule, wanampenda huyu hawataki hata astaafu. Umekuja na begi zima unaanza kuongea kauli za shoo shoo, umejibiwa na vitu viwili; salary slip na kitabu hiki chenye maslahi na mwongozo wa kazi za Mbunge. Unajiita Wakili Msomi, nami nili-post picha yako kabisa umevaa joho. Kaa ujitathmini, Taifa lilikuwa linakuhitaji, umeshajitia doa. Rudi kwa Mungu wako, rudi kwa wazazi wako, rudi kwa viongozi wako, chutama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli mimi niseme naunga mkono Azimio la Kamati, lakini adhabu ni ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa suala alilolifanya Gwajima ni uhaini. Sisi kama Watanzania tunayemwamini Rais wetu, mimi kama Mwanachama wa CCM ambaye namwamini Mwenyekiti wangu, anapaswa kupewa adhabu. Kama anaona Uaskofu ni mkubwa, atuachie Ubunge wetu. Wapo wana-CCM wengi mahiri wa kuweza kuleta maendeleo makubwa. Kawe ilicheleweshwa chini ya upinzani, tunataka iende mbali. Kwa hiyo, naomba adhabu iwe ya juu kabisa kwenye Bunge na pia hatua nyingine za kinidhamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kama vijana tunaipenda nchi hii, hatuko tayari kuona mtu yeyote akikwamisha juhudi za Serikali yetu chini ya Rais ambaye kwa kweli siku zote mama huyu hakuchukua fomu kugombea Umakamu wa Rais; Mama huyu hakutaka Urais, alimsindikiza mgombea wake wa Urais kunadi Ilani ya Chama. Yaliyotokea ni ya Mwenyezi Mungu. Ndiyo maana tunasema ni chaguo la Mungu, hana kundi huyo. Kwa hiyo, tunaomba kwa kweli adhabu ziwe kali mno na baada ya hapo vyombo vingine vya mamlaka viwape adhabu. Hakuna lingine. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Umesahau kutoa hoja tu. (Kicheko)

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii. Nianze kwanza kuipongeza Kamati yangu ya Nishati na Madini chini ya Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Dunstan Kitandula. Kwa kweli tumefanya kazi kubwa sana na tunashauriana na Serikali ili sekta yetu ya nishati na madini iweze kuwa na tija katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kwenye ushauri ambao hasa ni endelevu. Kwa kweli shirika letu hili la TANESCO ni kubwa mno na nishati yetu hii ya umeme inahitaji mipango mikakati ambayo ni endelevu. Leo hii Taifa letu ambalo tayari tumeshaanza kuchochea uchumi wa viwanda tuna umeme wa Megawatt 1,600 na tunajiona kwamba tuna umeme wa kutosha na wa ziada, lakini ukienda duniani na kujifunza utaona tuko nyuma sana na tumechelewa kujipanga vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii nchi ya Afrika Kusini ambayo ina population ya watu takribani milioni 59.3 ina uwezo wa kuzalisha umeme Megawatt 52,000 na bado wananunua umeme kutoka nchi Jirani ya Msumbiji na Namibia. Kwa hiyo, ukiangalia Rule of Thumb, kwenye nchi ya Afrika Kusini moja tu, kwamba Megawatt 1,000 ni sawa sawa na watu milioni moja, huo nindiyo uwiano wa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi leo katika nchi yetu tuko takribani milioni 60 lakini tuna umeme ambao ni Megawatt 1,600 na tukiona namna tulivyojipanga ni kwamba 2025 tunategemea kuwa na Megawatt 5,000. Mwaka 2044 tunajipanga kuwa na Megawatt 18,000. Sasa tukajifunza kwa wenzetu na nchi hii ya Afrika Kusini, hivi tunavyoongea, wana hali mbaya ya umeme kuliko sisi. Leo South Africa wana mgao wa umeme na baadhi ya maeneo hakuna umeme kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia nature ya matatizo, tunafanana; uchakavu wa miundombinu na kutokufanya periodic maintenance ya hivi vituo vyetu vya kupooza. Kwa hiyo, naona kikubwa kwa shirika letu, napongeze sana uteuzi wa Mheshimiwa Waziri pamoja na MD wa TANESCO, tunaamini nyie ni vijana, basi hebu kaeni chini mtumie vipawa vyenu muweze ku-plan, kwa sababu Wagogo wanasema: “If you fail to plan, then you plan to fail.” Tunataka kwenda kwenye uchumi wa juu, wa viwanda, lazima tuwe na umeme toshelevu ili kuepuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye jambo lingine la kuzuia, huko tunakoenda kwenye planning, ushauri wangu mwingine kuna kitu kinaitwa live line technology. Kwa sababu tumeona, walitutangazia siku kumi ili wafanye marekebisho kwenye vituo, lazima wakate umeme. Ila dunia ya sasa hivi, kuna kitu kinaitwa live line technology; ni mfumo unaoruhusu uendelee na ukarabati wa umeme bila ya kukata umeme. Huko ndiko dunia ilipo. Najua ni gharama, lakini ni bora utumuke leo kwa gharama kubwa lakini kuokoa hasara kubwa ambazo tunaweza kuzipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naona ukitumia hii live line unaweza kubadilisha nguzo bila kukata umeme, unaweza ukaunganisha watu wapya bila kukata umeme, unaweza ukabadilisha vikombe bila kukata umeme, unaweza kubadilisha transformer bila kukata umeme, unaweza kufanya marekebisho na matengenezo kwenye vituo vya kupooza bila kukata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo nalo tuliangalie. Ni uwekezaji mkubwa, lazima tuwafunze wataalamu wetu. Yapo mashirika binafsi hapa hawana tu uwezo wa kifedha, lakini TANESCO ikikaa nao kuona namna gani ya kuwawezesha ili tuingie na sisi kwenye utaalam huo, haya matatizo yataweza kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nchini kwetu tuna tatizo kubwa la radi. Kuna baadhi ya maeneo yanakaa muda mrefu bila kupata umeme kwa sababu ya radi, lakini huko duniani kuna technology inaitwa comby Unit; kuna kifaa kinawekwa kwenye transformer…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja za Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii. Kilimo siyo lelemama. Kwa kuanza, naomba nimnukuu Mheshimiwa Waziri ukurasa namba mbili kwenye utangulizi namba nne. Anasema; “Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuanza utekelezaji wa mageuzi kwenye sekta ya kilimo kwa kuwekeza katika miradi ya muda mrefu na maeneo ya msingi ya kutatua changamoto za kilimo kuanzia shambani hadi sokoni na kuitekeleza dhana na falsafa ya msingi kabisa kwenye kilimo kuwa “kilimo ni uwekezaji wa muda mrefu.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumnukuu Mheshimiwa Waziri, mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. Tupo hapa Wabunge ambao tulikuwepo Bunge lililopita na Mabunge mengine nyuma. Tangu Mheshimiwa Rais Dkt. Samia aingie madarakani kwenye Serikali ya Awamu ya Sita, na kumteua Mheshimiwa Bashe, kwa mara ya kwanza bajeti ya mwaka 2022 tulipongeza kwamba kilimo kimepewa fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ni mashuhuda. Leo hii nilikuwa napiga hesabu ya asilimia mpaka ikabidi niwaulize wenzangu, fedha za miradi ya maendeleo, tuliwatengea shilingi bilioni 569, zimekwenda shilingi bilioni 470. Pamoja na kasoro ambazo amezitoa mwenzangu, najua majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri yatakuja. Ni asilimia 82 na nukta. Haijawahi kutokea! Jamani, tupigeni makofi na tumpongeze sana Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri kwa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bashe amekuta kilimo kipo ICU (Intensive Care Unit), ameomba pesa kwa ajili ya madawa amtibu mgonjwa huyu, mwelekeo tunauona. Nchi hii tatizo kubwa ni kwamba tunao wakulima ambao kwa asilimia kubwa ni peasants. Hatuna farmers, tuna peasants. Sasa hawa mpaka uwanyanyue, na ubaya zaidi Mheshimiwa Waziri kwenye Wizara yake ana sera na mipango, lakini Waziri huyu hammiliki mkulima. Mkulima yuko Halmashauri kule kwenye TAMISEMI, ndiyo maana amekaa anabuni mambo ambayo sasa mwanga tunauona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe moyo Mheshimiwa Waziri, hata unaposikia hapa watu wanasema, ooh, itakuwaje? Umetupa forum ya kuongea, kwa sababu umedhubutu na unafanya. Leo tunaongelea kwamba kwa nini tunaingiza sukari? Kwa nini tunaingiza mafuta? Kwa nini tunaingiza unga wa ngano? Tumeona hizo nchi tunazotoa hayo mazao wamefanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge wa vijana, Mheshimiwa Ng’wasi, ametoa mfano wa nchi ile aliyoitaja, namna gani imeweza kuendelea kupitia mashamba haya makubwa. Kwa hiyo, kwa kweli napongeza hatua hizi, tena nampongeza sana Mkurugenzi wa Tume ya Umwagiliaji, Ndugu yangu Raymond. Kwa kweli moyo wa kilimo sasa upo kwenye tume yako. Ameongea Mheshimiwa aliyetangulia kuchangia kwamba tumepeleka fedha nyingi kuweka miradi ya umwagiliaji, weka mfumo mzuri wa usimamizi hii miradi iweze kuwa endelevu. Tunaona hatua nzuri ambazo mnazifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli kabla ya kwenda kwenye ushauri wangu kwanza, naomba niongelee Mkoa wangu wa Dodoma. Mimi kwa niaba ya Wabunge wenzangu wa majimbo, napenda kuwashukuru sana Wizara, mmetupendelea Dodoma. Sisi ndio tuna-pilot Mradi wa BBT pale Chinangali, na hapa ndiyo imeibuka sasa naiwaza hata Dodoma yenye utalii. Leo hii kutokana na jitihada zenu tunaenda sasa kuzungumzia kitu kinaitwa Agrotourism. Leo kwenye shamba lile la Chinangali nimeona Mheshimiwa Waziri mpango wako, pale kutakuwa kuna kiwanda cha wine, pale kutakuwa kuna restaurant, na uzuri umewaza kuweka private sector. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Msalato ikikamilika, mtalii akitoka nje, anashuka pale, anakuja Ikulu kuangalia, maana Ikulu tuna hadi wanyama mle, na pia atapita kwenye shamba lile kufanya Agrotourism. Vile vile ataenda Kondoa, tunayo michoro ya Kolo, tunayo Mkungunero kule, halafu ndiyo hapo ataenda Tarangire na Serengeti. Kwa kweli naunga mkono na ninawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na miradi ya BBT kugusa kule Chinangali, Bihawana, Membe na Chemba kule Gwandi, pia miradi ya umwagiliaji tumeipata Chamwino zaidi ya mmoja. Tumepata kule Bahi, Mpwapwa, Dodoma Mjini, Chemba, hata Wilaya ya Kondoa imeguswa, lakini cha kusikitisha tu, kule Kondoa mmegusa Kisese tu ambayo ni Kondoa DC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina salamu kutoka kwa wananchi na vijana wa Kondoa Mjini, wanasikitika, mbona wao hujawakumbuka Mheshimiwa Bashe? Wanafahamu kwamba Diwani wao wa Kondoa TC ndiye Makamu Mwenyekiti wa Kamati hii. Naomba kule kwenye Halmashauri ya Kondoa Mji tunayo Mongoroma Irrigation scheme kwenye Kata ya Seria ambayo ina zaidi ya ekari 3,000. Tunayo Mlangu Block Farm Kata ya Seria zaidi ya ekari 1,000; tunayo King’ang’a Irrigation Scheme, Kata ya Kingare zaidi ya ekari 3,000. Ukija kujumuisha, naomba ukawaguse vijana hawa wa Halmashauri ya Kondoa Mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafanya kazi kwa ukaribu kupitia Kamati, mimi nimshauri tu Mheshimiwa Waziri kuhusu mbegu. Naomba angalia namna ya kuwahusisha wakulima wadogo kwenye kuzalisha mbegu, na pia kwenye sekta binafsi. Huyu ASA nashauri abaki kwenye utafiti, abaki kuwa mdhibiti wa ubora wa hizi mbegu. Hebu kundi kubwa hili la private sector ulipe; tunao wawekezaji wazuri sana ambao wataweza kuwekeza na kuzalisha mbegu zilizo bora, wewe ukabaki kwenye kufanya tafiti na kudhibiti ubora wa hizo mbegu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona pia kupitia uwekezaji mkubwa wa kwenye umwagiliaji. Leo hii kwa sababu hawa Maafisa Ugani wanasimamiwa na Wakurugenzi. Tumeona changamoto, wamepeleka vifaa lakini ufanisi wa vile vifaa hatuuoni, kwa sababu hauna usimamizi. Umeenda mbali Mheshimiwa Waziri, umewaza kupitia hii Tume ya Umwagiliaji, umeajiri wataalam 320, umeenda kujenga ofisi 121, na pia tumeona mmekabidhiwa magari pale na Mheshimiwa Rais. Hii yote umeona namna gani unaweza kuongeza usimamizi ili sasa uende ukawaguse wakulima wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaambie wakulima wadogo, mimi ni mkulima mwenzenu, hamjaachwa kuwa wanyonge. Ndiyo maana katika malengo ya Wizara hii, ni kupunguza umasikini kwa asilimia 50 ifikapo 2030? Nani wa masikini? Ni nyie. Mipango ipo dhabiti, na ndiyo maana Mheshimiwa Waziri ametafuta mfumo mzuri wa kuwafikia na kuwasimamia, na kwa kweli tunamuunga mkono na tunajua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala hili linaongelewa kuhusu hii BBT. Jamani niwaambie, tunataka kuzalisha ajira mpya milioni tatu. Mnasema tukawafuate wale ambao wako kwenye kilimo, tunataka kutengeneza. Naomba nitoe ushuhuda. Mimi nilimaliza chuo mwaka 2009, nilienda kujiajiri kwenye kilimo. Nilikuwa msomi wa degree na nilikuwa mtoto wa kishua. Kwa jina langu tu ningeweza kutumia mazingira yangu kupata ajira, lakini nami nasema, natamani nijirudishe umri nyuma. Kipindi kile angekuwepo Rais Samia na Waziri Bashe, nami ningekuwa mnufaika wa hii BBT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu alitengeneza terminology ili kuvutia education, akasema education is sex. Mheshimiwa Bashe na Msaidizi wako Mavunde na wote Katibu Mkuu, Naibu Katibu na timu nzima, you are making agriculture sex, ili sisi vijana ambao ni kundi kubwa tuvutiwe na kilimo tuweze kwenda kuinua maisha yetu na tuweze kwenda kuanzisha matajiri wazawa ndani ya nchi yetu, ambao ni matajiri kupitia kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Katika nchi yetu kwa kweli kilimo kinafanyika sana, na ndiyo maana kwenye takwimu za Serikali tunaelezwa kwamba kilimo ndiyo ambayo imeajiri asilimia kubwa ya Watanzania. Cha kushangaza, miaka yote pamoja na jitihada kubwa za Serikali yetu, lakini mkulima anakutana na Serikali baada ya kuvuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kilimo ni mfumo wa mambo yafuatayo: Kilimo ni utafiti na utaalam (expertise), kilimo ni sayansi teknolojia na mitambo, kilimo ni udongo ama ardhi, kilimo ni mbegu, kilimo ni maji kwa maana ya mvua ama umwagiliaji, kilimo ni urutubisho, kilimo ni madawa, kilimo ni miundombinu ya uvunaji, kilimo ni miundombinu ya uhifadhi na mwisho kabisa, kilimo ni soko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mtitiriko ukikosea jambo moja tu, tayari umeshaondoa tija kwenye kilimo. Nasi kama Wabunge kila siku tunapiga makelele, tunataka kilimo cha nchi hii kiwe na tija. Kwa hiyo, kwa mara ya kwanza nimeshuhudia tangu niwe Mbunge, hii ni bajeti ya kwanza haijawahi kuambiwa kwamba ni ndogo kwa kilimo. Kwa hiyo, nimpe pongezi Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, ama hakika ameonyesha kwamba yeye ni mwanakilimo kwa vitendo; kwanza kwa kututeulia watu ambao wametupa matumaini, wanakuja kukivusha kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bashe alikuwa Naibu Waziri, meno yalikuwa madogo, sasa ana meno kama ya mamba ya kuja kuendeleza kilimo. Vile vile msaidizi wake Anthony Mavunde, ama hakika hii ni hazina yetu sisi Dodoma. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, haleluya!

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Ni mtu ambaye kila unamweka lazima aoneshe vitendo. Kwa hiyo, mimi nawapa shime muende mkayafanye, lakini Mheshimiwa Waziri angalia sana watu wa chini. Ninyi viongozi mna commitment, lakini huku chini hasa kwa Maafisa Ugani, nendeni mkaweke mechanism ya kuangalia utendaji wao, watakuja kuwaangusha. Kwa hiyo, lazima mwangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimekuwa mkulima kwa muda mrefu, na-declare interest. Naweza kuwa na shamba zaidi ya heka 1,000. Kwenye eneo husika sijawahi kuona hata siku moja Afisa Ugani akija hata kuomba mbegu tu niweze kuwapa wananchi wanaonizunguka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hawa watu tulioenda kuwapa vifaa, tumeona Rais wetu ameenda kweli sasa kuongeza utaalam, kawapa pikipiki, kawapa vifaa vya kupimia udongo, nendeni mkawasimamie ili wa-translate yale maono yenu. Unless otherwise they are going to fail you. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza bajeti imepanda 45.7 billion, hiyo ni hatua kubwa sana. Tumeonga mme-involve vijana. Niliwahi kushauri vijana lazima watengenezewe mazingira ya kushiriki kwenye kilimo. Naona sasa kwa mipango mliyokuwanayo, ama hakika kundi kubwa la vijana ambalo nimekuwa mtetezi wao siku zote, sasa wanaenda kushiriki kwenye kilimo kwa uadilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti ya umwagiliaji, siku zote bajeti inaenda kwenye kujenga mabwawa, lakini mmeenda mbali, mmeenda kutoa mpaka vitendea kazi. Naomba tu mjifunze, kule Egypt wanatumia River Nile kulisha karibu robo ya dunia, lakini River Nile source yake ni Lake Victoria. Sisi tuna mto, mpaka ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage jana kaongelea Ngono Project. Hebu tuangalie hii mito tuliyokuwanayo; Kagera na Morogoro tunaitumiaje? Tusiende kuchimba mabwawa ya irrigation scheme wakati tuna mito ambayo miezi 12 ina-flow bila kukatika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikienda kwenye mawazo yangu manne: Naomba tuanze sokoni. Leo hii uhaba wa mafuta umekuja kugundulika kupitia viwanda na biashara, lakini source ya upungufu wa mafuta ni kwenye kilimo. Kwa hiyo, naomba Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda na Biashara m-synchronize, mkae chini, mpange kwa pamoja. Leo hii India, nchi ambayo inaongoza kwenye kilimo, mkulima haendi kulima mpaka viwanda na biashara viseme msimu tunaoenda, ni zao gani litakuwa na soko zuri? Wanashauri watu wa kilimo, nao wanaenda kuwaambia wananchi wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, nilienda kutafuta soko la green beans. Tukakuta kuna watu kutoka Malawi nao wameleta green beans. Yale ya Malawi yalikuwa na size moja, yana rangi imependeza, kwa kweli tulipigwa, ila basi tu kwa vile tunaipenda nchi yetu, tukayala. Hawa sijui wanaweka madawa, wanaweka nini, lakini kitu cha kwanza ni appearance. Kwa hiyo, naomba sana, watu wetu wa viwanda na biashara, shirikianeni na Wizara ya Kilimo ili tuanzie sokoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna kitu kinaitwa agricultural zones. Nimekuwa nikipigia kelele kila nikichangia. Hata kipindi cha Hayati Mwalimu Nyerere ilikuwa hivyo, ndiyo maana kusini walikuwa wanalima korosho; ukija Tanga kuna Mkonge. Zao humea sehemu yoyoye, lakini linamea kwa ubora? Kuna mwaka watu walileta mikorosho huku Dodoma, imeishia wapi hiyo mikorosho?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona mmeweka clusters that is the way to go. We don’t have enough resources. Hatuna resources za kutosha, sasa utatawanya hizo resources zote? Bora ukiziweka sehemu moja zitaenda kufanya kazi kwa weledi na vizuri ili tuone matokeo na tija katika kilimo chetu tunachokifanya, lakini tusiache sayansi na teknolojia Mheshimiwa Waziri. Lazima tuende sawa na dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna kitu kinaitwa genetic modified seeds, tunazikataa kwa nini? Leo hii tunalima pamba, tunataka tuzalishe nguo, lakini katika nchi kumi zinazozalisha pamba hatumo. Nchi zote kama Brazil, India, China wanatumia GM Cotton Seeds. Sisi tunachotaka, tuleteeni hizo teknolojia halafu mkulima mwenyewe aamue. Leo mnasema oh, sijui zina madhara, ni uongo mtupu. Hayo ma-apple tunayoingiza kutoka nje mbona mbegu ndiyo hizo hizo zinatumika!

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe tu taarifa mzungumzaji kwamba suala la GMO ni tofauti anavyotaka kulichukulia. Kile ni kifo unachokula mwenyewe ukiona. Siyo sumu, ni kifo unachokula unakiona. Kwa hiyo, suala la GMO lina utata mkubwa na ni jambo siyo katika nchi yetu kuanza kulijadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mariam Ditopile, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hiyo taarifa. Hata simu zilipoanza walituambi oh, mionzi, hamtazaa. Simu tunatumia mpaka leo na zinarahisisha kazi zetu. Tusiogope sayansi. Leo hii kuna watu wanapata mimba bila hata kuingiliwa, wanapandikiza. Hiyo ndiyo sayansi, usibishane na sayansi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri, kusema ukweli mmefanya jitihada kubwa kupunguza riba za kwenye mikopo, lakini niseme ukweli, mkulima hakopesheki. Leo hii mimi ni mkulima lakini vilevile nina kiwanda cha kukamua mafuta ya alizeti. Nilienda kuomba mkopo Benki ya NMB, walikuja pale kwenye ghala langu wakakuta nina dumu za mafuta za lita 20 zaidi ya 2,000, nina stock ya kutosha, lakini walishindwa kunipa mkopo wakiniambia kwamba nyumba yangu moja hapa Dodoma Mjini ndiyo niiweke dhamana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mariam, malizia point yako, kengele imeshagonga.

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi mengine nitaenda kuyachangia kwa maandishi. Niwape moyo, niwatie nguvu, kwa kweli tunaenda kwenye the right direction. Mimi kama mkulima na Mbunge wa muda mrefu ambaye nimekuwa nalia na kilimo, sasa tunasema dalili ya mvua ni mawingu, mawingu tumeyaona na sasa tunaona zile rasharasha. Naamini mvua kubwa inakuja.