Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Mariamu Ditopile Mzuzuri (5 total)

MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi. Swali langu, je, kwa tafiti ambazo zimefanywa nchi nyingi sana, ikiwemo kwa nafasi kubwa nchi za Kiarabu, sigara ina madhara makubwa, mara dufu kuliko hii Shisha na kila siku tunasema ajira, ajira. Biashara ya Shisha ilikuwa inaajiri vijana wengi sana na kweli wamepata matatizo tangu hili zuio.
Swali langu kwa Serikali; je, mlifanya utafiti wa kutosha wa kuona kwamba hii Shisha ina madhara makubwa kuliko sigara? Nashukuru. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mariam kwa kutaka kujua kuhusu utafiti wa jambo hili. Nimhakikishie tu kwamba jambo hili lilifanyiwa utafiti na Wizara ya Afya na hivi vitu ambavyo vina vilevi, ubaya wake ni kwamba vijana wetu hawavitumii peke yake, wanachanganya na vitu vingine, kwa hiyo, wanaongeza makali zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira, nimhakikishie Mheshimiwa Mariam kwamba vijana bado wana fursa nyingi sana na nitolee mfano wa kwake yeye mwenyewe, ni mmoja wa vijana wanaofanya vizuri sana kwenye kilimo na yeye ni shahidi na amefanikiwa sana; ni mmoja wa Waheshimiwa Wabunge vijana waliofanikiwa sana kwenye kilimo. Kwa maana hiyo, vijana wengine wanaweza wakaiga mfano ule, wakalima mazao ya biashara. Mheshimiwa Mariam analima ufuta, wao nawakaribisha walime alizeti ama mazao mengine yanayostawi katika mikoa yao ili waweze kufanya biashara iliyo halali isidhuru maisha ya watu wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira ya kudumu, ndiyo maana Mheshimiwa Rais ana mpango wa muda mrefu wa kukuza uchumi kwa kuhakikisha kwamba fedha zote zinatumika vizuri ili kuweza kutengeneza uchumi wa viwanda, uchumi unaojitegemea, uchumi unaotengeneza ajira nyingi ambazo zitakuwa zinaingiza kipato halali kwa vijana na afya za Watanzania.
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo yana tija kwa vijana wa Mkoa wa Dodoma; na kwa vile yeye mwenyewe ni mtu sahihi, ni Waziri kijana, ni kijana na ni Mbunge anayetokana na Mkoa wa Dodoma, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, moja ya mazao ya biashara yaliyoonyesha kuwa na tija kwenye kilimo biashara Mkoa wa Dodoma ni pamoja na zao la zabibu, lakini mara baada ya Dodoma kutangazwa kuwa Makao Makuu ya Nchi, wageni wengi hususan kutoka katika nchi jirani za Afrika Mashariki, wameonekana kuvutiwa na uwekezaji kwenye zao la zabibu kama zao la biashara. Je, Serikali haioni umuhimu wa kutenga ardhi na pembejeo kwa vijana wa Mkoa wa Dodoma ili wawezeshiriki rasmi kwenye Sekta ya Kilimo cha Biashara kwenye zao la zabibu? (Makofi)

Swali la pili. Kwa kuwa kuna vijana tayari wamejiajiri kwenye ujasiriamali wa mazao, hususan katika zao la biashara la ufuta, lakini hivi karibuni kumetokea sintofahamu kwa Mkoa wa Dodoma hasa kwenye Wilaya ya Kondoa kuwazuia vijana hawa wasinunue ufuta kutoka kwa wakulima kwa kisingizio cha kuwa na stakabadhi ghalani, jambo ambalo halipo katika Mkoa wa Dodoma:-

Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusu vijana hawa ambao wameamua kujiajiri?

Mheshimiwa Spika, nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTONY PETER MAVUNDE): Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge Mariam Ditopile kwa namna ambavyo anawasimamia vijana wa nchi yetu ya Tanzania na hususan Vijana wa Mkoa wa Dodoma. Mwenyezi Mungu akubariki sana.

Mheshimiwa Spika, ni kweli, baada ya tangazo la Makao Makuu na pia baada ya Serikali ya Awamu ya Tano sikivu kufanya marekebisho katika ule mchuzi wa zabibu ili kuwavutia zaidi wakulima wa zabibu kuendelea kuilima zabibu, mwamko umekuwa mkubwa kwa vijana na kama Serikali mkakati wake katika eneo hili ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza, yalitoka maelekezo mwaka 2014 kutoka kwa aliyekuwa Waziri Mkuu wa wakati huo Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, ya kila Halmashauri nchi nzima kutenga maeneo maalumu kwa ajili ya shughuli za vijana kufanya kilimo. Kwa Mkoa wa Dodoma na hasa katika maeneo ambayo yanalima zabibu, tayari maelekezo yalishatoka na katika master plan ya Jiji la Dodoma, ambayo itakwenda kukamilika hivi karibuni, yametengwa maeneo maalumu ya kuhakikisha kwamba zao hili la zabibu halipotei.

Mheshimiwa Spika, hivyo, vijana pia watapata fursa ya kuweza kunufaika kupitia maeneo hayo ili nao waweze kulima zabibu na kujiongezea fursa ya kuendeleza mitaji yao na biashara zao.

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi kuliko yote ni kwamba, Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika maeneo yake ambayo wametenga kwa ajili ya shughuli za vijana, wameshapeleka wataalam kwenda SUA kukaa na wataalam wa SUA kwa ajili ya kuja na mpango mzuri endelevu wa kilimo cha zabibu ambacho kitakuwa kimefanyiwa utafiti ili vijana wengi zaidi waweze kunufaika.

Mheshimiwa Spika, siyo zabibu tu, kwa Dodoma hapa, vijana wengi hivi sasa wanafanya biashara za mazao, kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema; na hivi sasa tayari tunavyo viwanda ambavyo vimeanza kufanya kazi. Kwa mfano, Kiwanda cha Mazao Mchanganyiko ambacho kwa mwaka kitahitaji tani 12,000 za mahindi na tani 6,000 za alizeti. Kwa hiyo, tunachukua fursa hii pia kuwaalika vijana kushiriki katika kilimo hicho.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la Mheshimiwa Mbunge, analijibu Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo ambaye ameandaliwa kwa ajili ya kulijibu swali hilo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nichukue nafasi hii kumpongeza Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo ameyatoa. Ni kweli kabisa kumetokea sintofahamu katika zao la ufuta katika maeneo mengi hapa nchini na hasa katika mikoa ambayo inazalisha kwa kiwango kikubwa sana. Utaratibu ambao tumeweka kama Serikali, ni kwamba tunatumia ule utaratibu wa mwaka 2018 wa kuhakikisha, mtu yeyote anayetaka kununua ufuta, anaruhusiwa kwenda kununua maadam afuate taratibu zinazostahili; na wote wanaruhusiwa na hatujaweka masharti yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kumetokea katika baadhi ya mikoa, wanasema kwamba tunatumia mfumo wa soko la bidhaa yaani TMX na kuna maeneo mengine wanalazimisha kwamba wanaoruhusiwa ni hawa, hatujaweka huo utaratibu. Kila mtu anaruhusiwa kwenda kushiriki na huo utaratibu wa soko la bidhaa utakapokamilika, tutatoa elimu ya kutosha kwa wananchi ili kuanza kutumia huo mfumo. Kwa mwaka huu kwa sababu mfumo hatujaukamilisha sawasawa, basi mfumo wa zamani unaendelea kutumika.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza niipongeze Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na Wizara ya Kilimo; kwa kweli wakulima wa alizeti wameona neema kubwa sana. Hivi tunavyoongea bei ya mbegu ya kilo moja ya alizeti ni 1600, haijawahi kutokea katika nchi yetu. Kutokana na bei hiyo kupanda na kuleta matumaini makubwa sasa muamko umekuwa mkubwa kwa watu kwenda kulima alizeti.

Je, Serikali kupitia Wizara ya Kilimo imejipangaje kutuletea mbegu nyingi za kutosha na za kisasa ili tuweze kulima zao hili kwenye msimu unaokuja hasa kwa Mkoa wetu wa Dodoma?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ditopile kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali sasa hivi tumeanza kuchukua mahitaji ya mikoa wanayotuletea wao wenyewe kutokana na uwezo wa mkoa husika katika suala la uzalishaji. Katika mkoa wa Dodoma tunashirikiana kwa karibu kabisa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na RAS ambayo ina-coordinate kutuletea mahitaji ya kila Wilaya ili sisi kama wizara tuweze kuwapatia mbegu. Nataka niwahakikishie wakulima kuwa mwaka huu tutahakikisha wakulima wa alizeti wanapata mbegu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto zilizoko duniani za upatikanaji wa hybrid seed lakini at least tutahakikisha kwamba wakulima wote wanapata angalau standard seed ambazo zitaweza kuwasaidia katika mwaka huu na sisi Serikali wakati huo tunajipanga vizuri kwa ajili ya mwaka mwingine ili tuwe na hybrid za kutosha. Tumeshafanya aggregation tumeshaingia mikataba na wasambazaji na, hivi karibu tutaanza kusambaza mbegu kutokana na mahitaji ya mkoa husika.
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, kwanza niipongeze Serikali kupitia Wizara ya Kilimo kwani wamekuwa wanafanya programu nyingi sana za kumwezesha mkulima hasa wa alizeti. Lakini pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, mbegu bora ndio ambayo inazalisha zao bora, lakini changamoto kubwa ambayo inawapata wakulima wetu ni upatikanaji wa mbegu bora, lakini tuliona Serikali ikizindua mpango rasmi wa kugawa miche ya korosho kupitia Bodi ya Korosho katika Mikoa ya Kanda ya Kati, lakini sifa kubwa ya mikoa hii hususan Dodoma, Singida, Manyara na baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Morogoro ni mikoa ambayo inazalisha alizeti bora sana. (Makofi)

Je, Serikali kwa nini haioni sababu yak ama walivyogawa mikorosho, wawe na programu maalum ya kugawa mbegu bora za alizeti kwa mikoa hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, niipongeze Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, hususan Naibu Waziri wetu Mheshimiwa Hussein Bashe, amekuwa ni msikivu na kutatua changamoto zetu kwa haraka. Wamefuta mfumo wa kuuza mazao kwa mfumo wa TMX ambao kwa kweli ulikuwa kero kubwa sana kwa wakulima wetu, lakini pia hawaoni haja ya kusitisha pia mfumo wa stakabadhi ghalani, hususan kwa mikoa ambayo bado hawana miundombinu na mfumo mzuri kwa ajili ya stakabadhi ghalani?

Mheshimiwa Spika, mfano mzuri hapa Mkoa wetu wa Dodoma, Wilaya za Chemba, Bahi na Kondoa ambao tunazalisha sana ufuta na choroko, hatuna AMCOS, hatuna uongozi wowote. Kwa nini wasitoe muda ili tuweze kujiandaa tuunde mifumo mizuri halafu ndio tuweze kuanza kutumia mfumo huu wa stakabadhi ghalani? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mariam Ditopile wa Mzuzuri.

Mheshimiwa Spika, kwa nini tusigawe mbegu za alizeti kama ambavyo tuligawa miche ya korosho?

Mheshimiwa Spika, sababu ya Serikali kugawa miche ya korosho kwa wakulima katika mikoa ambayo ni mipya ya uzalishaji wa korosho ama michikichi sababu ya kwanza ni zao la korosho na zao la michikichi return on investiment kwa mkulima inachukua muda mrefu sana. Ukiangalia korosho mpaka mkulima aanze kupata mapato ni baada ya miaka mitatu, kwa hiyo, mfumo wa ku-finance input inakuwa kidogo ni gharama kwa mkulima na inakuwa inamuingia gharama nyingi, kwa hiyo, Serikali iliamua kuchukua hiyo hatua, ili kuweza kumpunguzia makali ya kununua miche na kuihudumia kwa kipindi cha miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwenye alizeti hatua ambayo tunachukua kama Serikali nikiri kwamba upatikanaji wa mbegu bora imekuwa ni changamoto na gharama ya mbegu inayopatikana ni kubwa kwa hiyo, mkakati wa Wizara ya Kilimo na mtakuja kuona kwenye bajeti yetu mwaka huu, Inshallah Mungu akijalia, ni kwamba tunawekeza katika mashamba ya Serikali, mifumo ya umwagiliaji. Na kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi kwamba ASA tutawapatia fedha kiasi cha shilingi bilioni 10. Hatua ya kwanza tunayoichukua ni kufanya jitihada na mwaka huu tumeanza kuishusha bei ya mbegu ya alizeti kutoka 35,000 ambayo wanayo sasahivi mpaka angalao shilingi 17,500 kwa kilo mbili kwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, nah atua hii tunaifanya kwa kuiwezesha ASA na mwaka huu imefanya pilot project. Imeuza mbegu zake za aina ya OPV ambazo uzalishaji wake wa mafuta hauna tofauti na mbegu ya high breed inayouzwa na kampuni binafsi kwa shilingi 35,000.

Kwa hiyo, tunaamini kwamba, kwa kuisaidia ASA itatusaidia kupatikana mbegu ya kutosha na tutasambaza kwa wakulima na katika bajeti yetu kuna mikoa ambayo ni ya uzalishaji wa alizeti ambayo tutaitaja katika bajeti ambayo tutaifanyia majaribio ya kupata mbegu, lakini vilevile tutaifanyia majaribio ya mifumo ya kusambaza mbegu hizo kwa wakulima, lakini vilevile kuwafanyia majaribio ya end to end contract, ili mkulima kama hana fedha tutengeneze utaratibu utakaomhusisha mnunuzi, mkulima apate mbegu bora na aweze kuzalisha shambani na kumuuzia mnunuzi moja kwa moja.

Kwa hiyo, hatuwezi ku-committ hapa kwamba, tutagawa mbegu za alizeti bure, lakini tunachoweza ku- committ ni upatikanaji wa mbegu za kutosha, lakini vilevile kuishusha bei kutoka 35,000 mpaka 17,500 ama elfu 15 kwa kilo mbili.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la mfumo wa stakabadhi ghalani; kwanza ni vizuri nitumie Bunge lako Tukufu ikaeleweka. Stakabadhi ghalani ni maelekezo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi, hili ni jambo la kwanza, lakini la pili stakabadhi ghalani ni mfumo ambao unasaidia kupatikana kwa bei halisi ya zao (price discovery). Ndio lengo la uwepo wa mfumo wa stakabadhi ghalani kwa ajili ya ushindani.

Mheshimiwa Spika, lakini ili uweze kutekeleza mfumo wa stakabadhi ghalani kuna mambo ya msingi ambayo ni lazima yawepo; la kwanza lazima kuwepo kwa chama cha msingi cha ushirika, ili wakulima waweze ku-aggregate, la pili lazima kuwepo na maghala, la tatu lazima kuwepo na wanunuzi ambao watashindana kwa uwazi.

Mheshimiwa Spika, ninakiri kwa niaba ya Serikali na Wizara kwamba yapo maeneo ambayo mfumo wa stakabadhi ghalani una changamoto. Na kama tulivyoamua kustopisha (stop) mfumo wa TMX tutasitisha katika baadhi ya maeneo ya nchi yetu kwa mwaka mmoja wakati tunajenga ushirika imara katika maeneo hayo, lakini maeneo hayo mfano Mkoa wa Dodoma, Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Singida, lakini Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Songwe katika maeneo haya hatuna ushirika imara, kwa hiyo, sasa hivi timu yetu inafanya kazi ya kupita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nitumie Bunge lako Tukufu kuwaomba Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa na Wakurugenzi katika mikoa hii kwa mwaka huu, hatua ya kwanza wanayotakiwa kufanya wachukue, wasajili wanunuzi wote wa mazao ya ufuta, choroko na, dengu katika maeneo yao na wawapatie leseni bure. Hatua ya pili wazuwie uuzaji wa mazao ya ufuta, choroko na dengu kwa kutumia madebe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivi, leo katika Wilaya ya Songwe mkulima anauza debe la kilo 14 kwa shilingi 20,000 ufuta, ambayo ni sawasawa na shilingi 1,400 average per kilogram, huu ni wizi, wakati FOB rate ya ufuta ni shilingi 3,000 katika port ya Dar Es Salaam. Kwa hiyo, tutatoa waraka na maelekezo ya namna ya kufanya, lakini Halmashauri ziwasajili wanunuzi bila kuwa-charge chochote, zianzishe point of sale katika kila kijiji na waweke mizani. Ni marufuku kuuza mazao ya kilimo kwa kutumia madebe na kufunga kwenye lumbesa. Nashukuru. (Makofi)
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, niseme wazi tu sijaridhika na majibu ya Serikali kwenye swali hili ambalo ni la mkakati na lina umuhimu sana na niseme tu mimi kama Mbunge mwenyeji nimeshafuatwa sana na Naibu Mawaziri huku kuwatafutia nyumba za kuishi na kwa kweli wanatusababishia mtaani watu wengi kukosa.

Mheshimiwa Spika, iliwezekana Dar es Salaam kule Masaki, kule Mikocheni kujengwa nyumba kwa ajili ya viongozi. Kwa nini ishindikane mbona mji wa Serikali tumeujenga? Kwa hiyo naomba kwa kweli nitakuja kulirudia hili swali na lije na majibu yanayoeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tumeona jitihada za Serikali katika ujenzi wa makao makuu katika kuendeleza miundombinu yetu.

Maswali mawili ya nyongeza; la kwanza naomba kuuliza je wamefikia hatua gani katika ujenzi wa airport ya kule Msalato? Lakini la pili katika ujenzi wa barabara ya mzunguko kwenye Jiji letu la Dodoma? Nnashukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, ahsante kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu maswali ya nyongeza mawili ya Mheshimiwa Mariam Ditopile kama ifuatavyo:-

Kwanza ni kweli kwamba Waheshimiwa Wabunge wameleta maombi mbalimbali ya nyumba pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali. Lakini tumeshatoa maagizo kwa Meneja Mtendaji Mkuu wa TBA na kuna viongozi wengine ambao walishastaafu yaani walikuwa Wabunge siyo Wabunge tena hapa Dodoma. Wengine walikuwa ni viongozi wa Serikali siyo viongozi wa Serikali walikuwa wanatumia hizo nyumba mpaka tunavyozungumza hapa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo wameshapewa notice nadhani ndani ya wiki mbili zijazo utapata taarifa halisi na baadhi ya Wabunge watapata nafasi ya nyumba hizi.

Mheshimiwa Spika, lakini maswali yake mawili kama ifuatavyo; la kwanza ni kweli kwamba Kamati ya kwako ya Kudumu ya Miundombinu, mwezi huu unaoishia walitembelea eneo la uwanja wa ndege wa Msalato, lakini pia na barabara za mzunguko hapa Dodoma naomba niseme tu kwamba fedha zipo za kulipa fidia. Pale Msalato kuna baadhi ya wananchi ambao hawakuwepo wakati wa fidia, fedha zipo zoezi linafanyika ndani ya muda mfupi sana zoezi litakamilika.

Mheshimiwa Spika, kujenga uwanja wa ndege wa Msalato pamoja na ring roads ni ahadi ya Serikali na Mheshimiwa Rais Mama Samia ameshatoa maagizo na maelekezo tutasimamia na itatekelezwa, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, lakini tumeona jitihada za Serikali katika ujenzi wa makao makuu katika kuendeleza miundombinu yetu.

Maswali mawili ya nyongeza; la kwanza naomba kuuliza je wamefikia hatua gani katika ujenzi wa airport ya kule Msalato? Lakini la pili katika ujenzi wa barabara ya mzunguko kwenye Jiji letu la Dodoma? Nashukuru.