Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Mariamu Nassoro Kisangi (2 total)

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa, mvua zimenyesha pasipo kueleweka, zimekwenda kuua mazao mengi sana katika maeneo mbalimbali, hali ambayo inaonesha kabisa kuna viashiria vya njaa huo mbele tunapokwenda. Je, Serikali yetu imejipanga vipi katika kukabiliana na janga kubwa la njaa ambalo linaweza kuja baadaye kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kisangi, Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kupitia swali hili kwanza naomba nitoe pole kwa wananchi wote ambao wamekumbwa na matatizo makubwa ya mafuriko. Mafuriko haya yameleta madhara makubwa ya vifo, uharibifu wa mali, lakini pia mashamba yetu yote yamesombwa na maji. Nilisema hapa nilipokuwa nahitimisha hoja yangu wiki iliyopita kwa kuwatahadharisha Watanzania baada ya kuwa tumepata taarifa kutoka chombo chetu cha hali ya hewa kwamba mvua hizi bado zinaendelea. Natoa pole kwa watu wa Kilosa, natoa pole kwa watu wa Moshi Vijijini na Rombo ambako pia ndugu zetu wengi wamepoteza maisha na madhara hayo ambayo nimeyataja.
Mheshimiwa Spika, Serikali imejipanga kuwahudumia Watanzania wote wanaopata madhara na mpango huu upo kwenye Ofisi yangu kupitia Kitengo cha Maafa. Tunaendelea kufanya tathmini na tathmini hii inafanywa kwanza na Halmashauri zote zote za Wilaya ambazo ndiyo zimeunda Kamati ya Maafa kwenye maeneo yao. Wakishafanya tathmini, Mkoa unafanya mapitio na mahitaji yao halafu wanatuletea ofisini kwetu; nasi tunapeleka misaada kadiri walivyoomba kwenye maeneo yao.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa tuna hifadhi ya chakula, yaani tunacho chakula cha kutosha cha kupeleka kwenye maeneo hayo na tayari tumeshaanza kupeleka chakula kwenye maeneo yote yaliyopata maafa. Tumejiimarisha tena kwa ajili ya maafa haya yanapoweza kutokea hapo baadaye na kutumia msimu huu wa kilimo kwa maeneo ambayo hayajapata madhara.
Nataka nitoe wito kwamba tulime sana, tupate chakula kingi tuweze kutunisha hifadhi yetu ya chakula ili pia tunapopata tatizo la mahitaji ya chakula, basi chakula hicho tuweze kukipeleka maeneo yote yenye maafa.
Mheshimiwa Spika, pia kitengo hiki sasa tunakiboresha, tunaanza mazungumzo ndani ya Serikali kuifanya kuwa agency ambayo itakuwa inaratibu shughuli zote za maafa popote nchini, ambapo tutakuwa tunatengea fedha ziweze kutafuta maturubai au vibanda vya kujihifadhi kwa muda mfupi lakini pia kununua vyakula, madawa na mahitaji mengine ili yanapotokea tu maafa kama haya, basi kitengo chetu kiende mara moja.
Kwa sasa tumejiimarisha vizuri, maeneo yote yenye maafa tumeshayapitia na wataalam wetu wapo huko kwenye maafa ili kunusuru maisha ya Watanzania wenzetu ambao sasa wamepata mahangaiko kutokana na mvua nyingi ambazo zimenyesha.
Mheshimiwa Spika, pia tahadhari kwa wale wote ambao wako kwenye mabonde, narudia tena, nataka niwasihi Watanzania wote ambao wako kwenye maeneo hatarishi wapishe maeneo hayo, watafute maeneo mazuri. Viongozi wa Serikali za Vijiji, Kata na Wilaya wawasaidie Watanzania hao kuwapeleka maeneo sahihi ili waweze kuepukana na madhara yanayoweza kujitokeza itakapotokeza mvua nyingi kunyesha tena ambazo zinaendelea kwa sasa.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, katika miezi ya karibuni katika Mikoa mbalimbali ya nchi yetu kumekuwa na changamoto kubwa ya kupanda kwa gharama za maji bila kuzingatia uasilia, kuletewa bili zisizo sahihi, kukatiwa maji bila utaratibu na kukosa maji kwa muda mrefu kisha unaletewa bili kubwa. Kero hiyo imejitokeza katika Mikoa mbalimbali katika nchi yetu ikiwemo Mikoa ya Dar es Salaam, Manyara, Dodoma, Tanga, Mwanza na Mikoa mingine mingi na hasa katika maeneo ya Mijini.

Je, Serikali inatoa kauli gani kwa wananchi wake waliokumbwa na kero hiyo?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Kisangi, Mbunge wa Mkoa wa Dar es Salaam, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, alichosema Mheshimiwa Mbunge, yako maeneo yanajitokeza kwamba mamlaka tulizozipa mamlaka hiyo ya kusimamia maji kwenye maeneo yao, tunazo mamlaka ambazo tunazianzisha sasa za RUWA za vijijini na kwenye ngazi za Wilaya, lakini zipo mamlaka ambazo zimechukua maeneo makubwa kwenye ngazi za Mikoa, pia tuna Kamati za Maji ambazo zinasimamia miradi hii kwenye maeneo ya vijiji na maeneo mengine yote.

Mheshimiwa Spika, kumejitokeza wimbi la mabadiliko ya bei. Ni kweli upo utaratibu ndani ya Serikali kwamba mamlaka hizo zinapoona zinahitaji kuboresha huduma zinaweza kufanya mapitio ya bei zao. Lakini kinachotokea sasa ni kwamba zipo mamlaka zinapita zaidi ya kiasi.

Mheshimiwa Spika, nimefanya ziara Mkoani Simiyu na hapa karibuni nilikuwa kwenye Wilaya ya Maswa, moja kati ya malalamiko niliyoyapokea kwa wananchi pale ni kupanda kwa bei kutoka shilingi 5,000 wanayoilipa kwa mwezi mpaka shilingi 28,000. Sasa bei hizi hazina uhalisia, hakuna sababu ya mamlaka kutoza fedha yote hiyo na kuwafanya wananchi wakose maji.

Mheshimiwa Spika, Serikali ndiyo inatekeleza hii miradi na inatoa fedha kwa lengo la kuwapa huduma wananchi ili wapate huduma ya maji. Mamlaka tumewapa jukumu la kusimamia mradi huo na kuhakikisha kwamba angalau wanaweza kufanya marekebisho, matengenezo pale ambapo kunatokea uharibifu. Kwa hiyo, gharama haziwezi kuwa kubwa kiasi hicho na wala wao hawapaswi kutoza wananchi ili kurudisha gharama za mradi kwa sababu Serikali haijadai gharama ya kuendesha mradi huo kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri jana nilikuwa na Waziri wa Maji nikimwambia hili la kwamba lazima afuatilie Mamlaka ya EWURA ambayo ina mamlaka ya kukaa na hizo mamlaka zetu za maji kufanya mapitio ya bei. Bei zinazotakiwa kuwekwa ni zile ambazo mwananchi wa kule kijijini anaweza kuzimudu lakini siyo kwa kupandisha bei kutoka shilingi 5,000 mpaka shilingi 28,000, jambo ambalo halina uhalisia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote na Watanzania kwa ujumla, tutaendelea kusimamia Mamlaka zote za Maji, lakini Serikali itaendelea kutoa huduma za maji, nataka tujiridhishe kila Mtanzania anapata maji kwenye maeneo yake kwa usimamizi wa mamlaka hizi, lakini hatutaruhusu na hatutakubali kuona Mtanzania anatozwa gharama kubwa za maji kiasi hicho. Huku tukiwa tunatoa wito kwamba lazima tuchangie maji ili tuweze kuendesha miradi hii pale ambapo tunatakiwa kununua diesel, tunatakiwa tununue tepu ya kufungulia maji au bomba linapopasuka, lazima mamlaka zile ziweze kufanya ukarabati huo, lakini siyo kwa kutoza fedha kiasi hicho.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, masharti ambayo yapo mnapotaka kuongeza bei ni kwamba mamlaka hizo zinapodhamiria jambo hilo ni lazima kwanza zitoe taarifa EWURA, mbili kwenye vikao hivyo lazima Kamati za Maji zihusike, Kamati ambazo zinaundwa na wananchi wenyewe, tatu ni lazima wahusishe wadau, wadau ni wale watumia maji. Kwa hiyo, wote wakikubaliana sasa kwa viwango ambavyo wananchi wake wanaweza kuvimudu ndipo mnaweza kupandisha. lakini msipandishe wenyewe na mkawaumiza wananchi na miradi yenyewe imetekelezwa na Serikali, Serikali inayotaka wananchi wapate maji halafu mnataka kuwakwaza wananchi wasipate maji waanze kuilalamikia Serikali yao. Hatutakubaliana na hili na kwa hiyo mamlaka ziwe makini, Wizara ya Maji iendelee na utaratibu na maagizo ambayo nimewapa jana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)