Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Sophia Mattayo Simba (2 total)

MHE. SOPHIA M. SIMBA aliuliza:-
Hali ya magereza nchini ni mbaya hivyo kufanya vigumu katika utoaji wa haki za kibinadamu licha ya kwamba nchi imekuwa ikijali sana utekelezaji wa mikataba mbalimbali ya kikanda na ya kimataifa katika utoaji wa haki hizo za wafungwa.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha hali hiyo katika magereza nchini?
(b) Je, Serikali imejenga magereza mapya mangapi katika kipindi cha miaka 20 iliyopita?
NAIBU WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Mathayo Simba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kuboresha hali ya magereza nchini kwa awamu kadri ya fedha zitakavyopatikana. Katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali imetenga fedha katika fungu la maendeleo na matumizi mengineyo kwa ajili ya ukarabati, upanuzi, ujenzi wa mabweni mapya, majengo ya utawala na ununuzi wa vifaa mbalimbali vya malazi katika magereza nchini ili kuboresha huduma kwa mahabusu na wafungwa kukidhi vigezo vya haki za binadamu.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miaka 20 iliyopita Serikali imejenga magereza mapya 11 kwa mchanganuo ufuatao:-
1. Gereza la Mkuza- 1996;
2. Gereza la Mbarali - 2003;
3. Gereza la Igunga - 2003;
4. Geeza la Meatu - 2003;
5. Gereza la Mgagao - 2004;
6. Gereza la Kinegele - 2005;
7. Gereza la Mbozi - 2005;
8. Gereza la Mbinga - 2007;
9. Gereza la Chato - 2008;
10. Gereza la Kiteto - 2009; na
11. Gereza la Karatu - 2010.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo magereza hayo pamoja na ujenzi kutokamilika yanaendelea kutumika isipokuwa Gereza la Chato na Gereza la Karatu.
MHE. SOPHIA M. SIMBA aliuliza:- Lugha ya Kiingereza ina umuhimu mkubwa katika majadiliano na wenzetu wa nchi nyingine na pia hutumika kufundishia katika shule zetu kuanzia sekondari hadi vyuo vikuu, lakini lugha hii imekuwa changamoto kubwa kwa wanafunzi katika masomo yao. (a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kufundisha lugha ya kiingereza kuanzia shule za awali na kuendelea ili Watanzania wawe na lugha ya pili inayotumiwa na watu wote? (b) Je, Serikali haioni kuwa wananchi wengi wanapenda kuongea kiingereza hivyo ione namna ya kuwawezesha?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Mattayo Simba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:- (a) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mfumo wa elimu wa Tanzania zipo shule za msingi za Serikali zipatazo 11 na zisizo za Serikali zinazotumia lugha ya kiingereza kuanzia darasa la awali ambapo lugha ya kiswahili hutumika kama somo. Vilevile sehemu kubwa ya shule za msingi za Serikali hutumia lugha ya kiswahili kama lugha ya kufundishia tangu awali na lugha ya kiingereza kama somo kuanzia darasa la tatu na kuendelea. Aidha, lugha ya kiingereza ni lugha inayotumika kufundishia shule za sekondari na vyuo vikuu kwa masomo yote isipokuwa komo la kiswahili. (b)Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inathamini mchango wa matumizi ya lugha ya kiingereza kwani hutumiwa na wananchi kama lugha ya pili katika kupata maarifa na ujuzi katika nyanja za uchumi, siasa, utamaduni, sayansi na teknolojia. Katika kuimarisha matumizi ya lugha ya kiingereza kwa walimu, kati ya mwaka 2014 hadi 2016 Serikali iliendesha mafunzo ya kuimarisha ufundishaji na ujifunzaji wa somo la kiingereza kwa walimu wapato 14,054 kupitia mpango wa Student Teacher Enrichment Programme (STEP). Pia kati ya mwaka 2015 hadi 2017 iliendesha mafunzo ya mitaala mipya kwa walimu wapato 82,186 ili kumudu stadi za ufundishaji wa masomo yote ikiwemo kiingereza. Aidha, kwa watu wazima wanaopenda kujifunza lugha ya kiingereza zipo taasisi ambazo hutoa mafunzo ya muda mfupi