Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Stella Ikupa Alex (19 total)

MHE. STELLA IKUPA ALEX aliuliza:-
Kumekuwa na ongezeko la ombaomba au utegemezi kwa watu wenye ulemavu nchini:-
Je, ni kwa nini Serikali isiwawezeshe kiuchumi watu wenye ulemavu kwa kuwapa upendeleo wa zabuni za kazi mbalimbali, kama vile kuzoa takataka, usafi wa vyoo, ushonaji na kadhalika kwenye Halmashauri?
NAIBU WAZIRI WA SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WALEMAVU (MHE. DKT. ABDALLAH S. POSSI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri Mkuu, napenda kujibu swali namba 61 la Mheshimiwa Stella Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua haki za watu wenye ulemavu kufanya kazi kwa misingi sawa na wengine, ikiwa ni pamoja na kuwawezesha kiuchumi, fursa za ajira na kuwaandalia mazingira wezeshi. Serikali pia inatambua uwepo wa watu wenye ulemavu waliojiajiri wenyewe kupitia makampuni au vikundi mbalimbali ambao wanahitaji kuungwa mkono ili kupambana na utegemezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuhakikisha upatikanaji wa fursa sawa kwa watu wenye ulemavu katika fursa mbalimbali, zikiwemo fursa za ajira na za kiuchumi, Serikali itaendeleza kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Watu Wenye Ulemavu, Sheria Namba Tisa (9) ya Mwaka 2010 inayoelekeza hatua za makusudi za msingi na wajibu wa kutambua haki za watu wenye ulemavu. Kifungu 34(2) cha Sheria tajwa kinaipa nguvu Serikali kuchagiza upatikanaji wa fursa za ajira kwa watu wenye ulemavu kwa kufuata utaratibu wa kutoa kipaumbele maalum (affirmative action).
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa umuhimu wa pekee Serikali inawasisitiza Watendaji wote kwamba kwa mujibu wa Kifungu cha tatu (3) cha Sheria Namba Tisa (9) ya Mwaka 2010, maana ya neno kubagua inajumuisha, kukataa bila sababu maalum kutoa kipaumbele maalum kwa watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nirudie, kwa mujibu wa Kifungu cha tatu (3) cha Sheria Namba Tisa (9) ya Mwaka 2010, maana ya neno kubagua inajumuisha, kukataa bila sababu yoyote kutoa kipaumbele maalum kwa watu wenye ulemavu. Hivyo basi, Watendaji wa Serikali wanawajibika kutoa kipaumbele maalum kwa watu wenye ulemavu katika masuala na fursa mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi Ibara ya 58(2) imeelekeza kutengea asilimia 30 ya tenda zote za utoaji huduma kwenye Halmashauri zote nchini kwa makundi maalum wakiwemo watu wenye ulemavu.
Viwanja vya ndege nchini ukiondoa uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere - Dar es Salaam havina miundombinu au huduma ya kubebea abiria wasiojiweza ikiwemo wagonjwa, wazee pamoja na watu wenye ulemavu.
(a) Je, Serikali haioni umuhimu wa huduma hii katika viwanja vingine nchini?
(b) Huduma hii imekuwa ikifanya kazi na wakati mwingine kuharibika katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere - Dar es Salaam, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha huduma hii inapatikana muda wote kwenye uwanja huu wa Mwalimu Nyerere?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, (a) Serikali kwa kutambua umuhimu wa kuwa na huduma kwa ajili ya wasiojiweza, wagonjwa, wazee pamoja na watu wenye ulemavu imeweka vifaa vya kubebea wagonjwa (wheel chairs na stretchers) katika viwanja vya ndege vya Mwanza, Mafia, Arusha, Tanga, Songwe na Mtwara; pamoja na lift kwa kiwanja cha ndege cha Bukoba. Juhudi za kuboresha miundiombinu au huduma hiyo katika viwanja vingine zinaendelea kadiri ya upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania imetenga fedha za ndani kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya viwanja vya ndege ikiwemo huduma ya wasiojiweza.
Mheshimiwa Naibu Spika, (b) naomba nishukuru kuwa Mheshimiwa Stella Ikupa Alex anatambua uwepo wa miundombinu au huduma kwa ajili ya wagonjwa, wazee pamoja na watu wenye ulemavu katika uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere. Aidha, naomba nimfahamishe kuwa huduma hizo zipo za aina mbalimbali kulingana na mahitaji. Baadhi ya huduma hizo ni pamoja na huduma zitolewazo katika lift, gari la wagonjwa (ambulance), viti vya magurudumu (wheel chairs) na gari lenye lift (ambulift). Aidha, haijawahi kutokea kuwa nyenzo zinazotumika kutoa aina hizo za huduma zimeshindwa kufanya kazi kwa pamoja.
Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere una chumba maalum cha maulizo ambapo mtu yeyote mwenye msafiri anayehitaji huduma maalum akifika katika chumba hicho atapata maelezo ya namna atakavyopata huduma anayoihitaji.
Tunatambua uwepo wa baadhi ya watu ambao hufika katika uwanja huo bila kusoma maelezo na hivyo, kushindwa kutambua wapi watapata huduma hiyo. Naomba kuwajulisha kuwa wafanyakazi wa mamlaka ya viwanja vya ndege mara wanapotambua uwepo wa mhitaji wa huduma malaam humsaidia.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-
Kumekuwa na uuzaji holela wa vifaa hatarishi barabarani kama vile visu, mapanga na kadhalika.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kukomesha biashara hii ambayo ni hatari kwa usalama wa wananchi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwa na uuzaji holela wa vifaa hatarishi barabarani. Vifaa hivi hutumika kwa shughuli mbalimbali kama vile kilimo. Hata hivyo vinaweza kutumika vibaya na kuhatarisha maisha ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ushauri kwa Halmashauri zetu zote na mamlaka zinazohusiana na biashara kutenga maeneo maalum na kusimamia vema biashara hizo. Aidha, kama hali hii itaendelea Serikali haitasita kuchukua hatua stahiki kukomesha biashara ambayo inaweza ikaleta hatarishi pindi itakapotumika vibaya.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-
Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 Sehemu ya Tatu, kifungu cha 8 kinaelezea uanzishwaji wa Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu na kifungu cha 13 kinazungumzia vyanzo vya fedha.
(a) Je, ni kwa nini baraza hilo halifanyi kazi kama sheria inavyoelekeza?
(b) Sehemu ya Tatu ya kifungu cha 14 cha sheria hiyo kinaeleza juu ya Kamati za Watu Wenye Ulemavu kuanzia ngazi ya kijiji; je, ni kwa nini Kamati hizo mpaka sasa hazijaundwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex , Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Baraza la Ushauri la Utaifa la Watu wenye Ulemavu limeanzishwa chini ya Kifungu cha 8 cha Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010. Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu lilizinduliwa rasmi tarehe 1 Novemba, 2014. Baraza hili limekuwa likifanya kazi ipasavyo kwa kujadili masuala ya watu wenye ulemavu kupitia vikao vyake ambapo kwa mara ya mwisho Baraza lilikutana tarehe 14 Januari, 2017.
Aidha, Baraza limekuwa likitekeleza majukumu yake kwa kuishauri Serikali kuhusu uboreshaji wa huduma za watu wenye ulemavu nchini.
(b)Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Watu wenye Ulemavu, kifungu cha 14(2) inaelekeza kuundwa kwa Kamati za Watu wenye Ulemavu katika ngazi ya Kijiji/Mtaa, Kata, Halmashauri hadi Mkoa.
Kutokana na kifungu hiki cha sheria, Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, imekwishatoa agizo kwa Mikoa na Halmashauri zote chini kuunda Kamati za Watu Wenye Ulemavu kwa mujibu wa Sheria ya Watu wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kuikumbusha Mikoa na Halmashauri ambazo hazijaunda Kamati za Watu Wenye Ulemavu kutekeleza agizo hilo kwani ifahamike kwamba kutokuunda kamati hizo ni ukiukwaji wa matakwa ya kisheria.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-
Asilimia kubwa ya watu wenye ulemavu wana vipato duni sana kiasi cha kushindwa kumudu ghamara za matibabu.
Je, Serikali haioni kuwa ni muda muafaka sasa wa kuwajumuisha Watanzania hawa wenye kipato duni na wenye ulemavu kwenye sera ya msamaha wa uchangiaji huduma za afya kama ilivyo kwa wanawake wajawazito, watoto chini ya miaka mitano na wazee?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimwia Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Sera ya Afya ya mwaka 2007 imeainisha makundi yanayostahili kupata msamaha wa kulipia huduma za afya katika vituo vyote vya kutolea huduma.
Kulingana na Sera hiyo, Serikali inatambua kuwepo kwa wananchi wasio na uwezo wa kuchangia gharama za huduma za afya, ikiwa ni pamoja na wale walio katika makundi maalum ya kijamii, mathalan Wazee walio na umri zaidi ya miaka 60 ambao hawana uwezo wa kipato, watoto wenye umri chini ya miaka mitano, watoto walio katika mazingira hatarishi, wanawake wajawazito na watu wasiojiweza kiuchumi. Pia watu wenye magonjwa sugu kama saratani, UKIMWI, kisukari, magonjwa ya moyo, pumu, sickle cell, kifua kikuu, ukoma na magonjwa ya akili. Madhumuni ya sera hii ni kuwezesha makundi maalum kupata huduma bora za afya sawa na wananchi wengine.
Mheshimiwa Spika, hivyo basi, napenda kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kuwa watu wenye ulemavu wamezingatiwa katika makundi ya watu wanaostahili msamaha.
Mheshimiwa Spika, aidha, msamaha kwa kundi hili utatolewa kwa kuzingatia kama mlemavu huyo atabainika kuwa hana uwezo wa kulipia huduma au kuwa katika moja ya makundi yanayostahili msamaha niliyoyataja.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-
Kutokana na umuhimu wa elimu jumuishi Tanzania (inclusive education).
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa kila mwalimu anapatiwa mafunzo maalum yatakayomuwezesha kufundisha wanafunzi wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imeandaa mtaala mpya ambao umeandaliwa katika misingi ya elimu jumuishi na ulianza kutumika kuanzia mwaka wa masomo 2014/2015. Hadi sasa wahitimu wa ngazi ya Stashahada ya Elimu Maalum wapato 158 wamehitimu Oktoba, 2016 na wanachuo 248 wanaendelea na masomo katika Chuo cha Ualimu Patandi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhumu wa walimu hawa, Wizara katika mwaka wa fedha 2016/2017 iliendesha mafunzo kwa walimu kazini 519 wanaofundisha darasa la kwanza na la pil kuhusiana na mtaala ulioboreshwa ili kumudu ufundishaji wa wanafunzi wenye mahitaji maalum. Vilevile tarehe 20 mpaka 28 Juni, 2017 walimu kazini 712 wanaofundisha wanafunzi wenye ulemavu wa akili na wenye usonji walipatiwa mafunzo katika vituo vya Mwanza, Arusha, Mbeya na Morogoro ili kuwajengea uwezo wa kumudu ufundishaji wa wanafunzi wenye ulemavu wa akili na usonji.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, walimu 600 wanaofundisha darasa la tatu na la nne watapatiwa mafunzo ya mtaala ulioboreshwa kuanzia tarehe 10 hadi 30 Julai, 217 lengo ni kuwafikia walimu wengi zaidi.
STELLA I. ALEX aliuliza:-
Kwa kuzingatia umuhimu wa taulo za kike nchini. Je, Serikali inaonaje ikiondoa kodi kwenye taulo hizo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO aliuliza:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, maombi ya kuondoa kodi kwenye taulo za kike yamewahi kuwasilishwa na watumiaji pamoja na wauzaji wa bidhaa hiyo.
Mheshimiwa Spika, mapendekezo na maazimio yametolewa katika vikao mbalimbali vya wadau na Serikali. Maamuzi ya suala hili yamechelewa baada ya kubaini kuwa bidhaa hii haikuwa miongoni mwa orodha ya vifaa vya matibabu (vifaa tiba) ambavyo huondolewa kodi isipokuwa zimeondolewa ushuru wa uingizaji (import duty) na aina nyingine za kodi zinalipiwa kama bidhaa nyingine zote.
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imewaandikia barua Wizara ya Fedha na Mipango kuona namna ya kuondoa kodi katika bidhaa hii. Majadiliano yanaendelea kuwezesha bidhaa hii iunganishwe katika orodha ya vifaa tiba ili viweze kupata msamaha wa kodi sambamba na vifaa vingine vya tiba. Hii itapunguza gharama za upatikanaji wake kwa kuziondolea baadhi ya kodi zenye kuongeza bei kwa kiwango kikubwa mfano kodi ya ongezeko la thamani (Value Added Tax).
MHE. STELLA I. ALEX aliuiliza:-
Je, ni lini Serikali itaanzisha miradi maalum itakayosaidia kupunguza ama kuondoa makali ya maisha kwa watu wenye ulemavu wasio na ajira maofisini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa watu wenye ulemavu kama kundi maalum katika jamii ambao wanakabiliwa na changamoto mbalimbali katika kuzifikia haki zao na fursa za maendeleo ikiwemo haki ya kupata mitaji kwa ajili ya kuanzisha miradi au shughuli za uzalishaji mali.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, katika kuwawezesha watu wenye ulemavu kujumuika katika shughuli za maendeleo na maisha ya jamii, Serikali imeweka mazingira yanayoruhusu ushiriki wao katika masuala ya jamii sawa na wasio na ulemavu ikiwa ni pamoja na kupata elimu na mafunzo ya stadi za kazi katika shule au vyuo jumuishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuhakikisha kuwa watu wenye ulemavu nao wanashiriki katika kuanzisha au kuanzishiwa miradi, Serikali kupitia Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, itaendelea kuhakikisha inaimarisha mifumo iliyopo ya kuhakikisha Watanzania wote wakiwemo watu wenye ulemavu wananufaika na mipango ya Serikali ya kuwawezesha kiuchumi. Hata hivyo, dhana ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanashirikishwa katika shughuli mbalimbali za maendeleo ni ya muhimu sana ili kuondoa unyanyapaa.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa Mikopo ya Elimu ya Juu kwa Watu wenye Ulemavu kama ruzuku badala ya mikopo kama ilivyo sasa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mikopo inayotolewa na Serikali kupitia Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu inaongozwa na Sheria ya Bodi ya Mikopo (SURA 178) ambayo inabainisha kuwa fedha na mikopo hiyo ni kwa ajili ya wanafunzi wahitaji (needy) wenye sifa za kujiunga na taasisi za elimu ya juu (eligible). Lengo la matakwa haya ya kisheria ni kuwawezesha wanafunzi wote wahitaji, wenye ulemavu na wasio na ulemavu, wanaotoka kwenye familia zenye uwezo mdogo wa kiuchumi kufikia ndoto zao za kupata elimu ya juu.

Mheshimiwa Spika, sheria pia inaipa Bodi mamlaka ya kuweka vigezo vya ziada ambapo katika mwaka wa masomo 2020/2021, Mwongozo wa Utoaji Mikopo ulitoa kipaumbele kwa makundi maalum wakiwemo wenye ulemavu au waombaji mkopo wenye wazazi wenye ulemavu. Kwa kutumia kigezo hiki, katika mwaka wa masomo 2020/ 2021, jumla ya wanafunzi 92 wenye ulemavu au wazazi wenye ulemavu walipangiwa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 350.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la kutoa ruzuku badala ya mikopo, Serikali italifanyia kazi kwa kuzingatia dhana nzima ya utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wenye uhitaji na kuwa na mfuko endelevu wa mikopo ya elimu ya juu nchini.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu mzuri wa matibabu kwa watu wenye ulemavu wakati ikisubiri Bima ya Afya kwa wote?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL). alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka utaratibu wa kuwatambua watu wenye ulemavu kupitia Kamati za Watu Wenye Ulemavu kuanzia ngazi ya kijiji na kuwaunganisha kwenye vituo vyetu vya kutolea huduma za afya kulingana na mahitaji yao. Aidha, kupitia mipango kabambe ya afya ya halmashauri Serikali imeendelea kuwatengea rasilimali kulingana na mahitaji yao. Mfano kwa walemavu wa ngozi wanawezeshwa mafuta ya kuzuia jua (Sun Cream) ambayo kwa sasa hutengenezwa katika Hospitali ya Kanda ya KCMC, na bidhaa hii imeingizwa kwenye orodha ya bidhaa za afya zinazosambazwa na Bohari ya Dawa (MSD).

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetoa miongozo ya miundombinu ya kutolea huduma kwa kuzingatia haki za watu wenye ulemavu. Pia, Wizara imeendelea kutengeneza miongozo na mafunzo kwa watoa huduma ili kuwezesha na kuboresha utoaji wa huduma kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mswada wa Bima ya Afya kwa Wote unakuja, hii ni fursa muhimu sana kwa sisi Wabunge kutengeneza sheria nzuri zitakazolinda haki za watu wenye ulemavu. Ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuingiza lugha ya alama kwenye mitaala ya elimu nchini?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu Swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa Lugha ya Alama katika kuondoa kikwazo cha mawasiliano kati ya wenye uziwi na wale wasio na uziwi. Katika kufikia lengo la kuingiza Lugha ya Alama kwenye Mitaala ya Elimu nchini, Serikali imekamilisha usanifishaji Kamusi ya Lugha ya Alama ya Tanzania ya mwaka 2020 na kurahisiha ufundishaji na ujifunzaji pamoja na mawasiliano. Vilevile, Serikali imekamilisha uandaaji wa Mwongozo wa Utekelezaji wa Mtaala wa Elimu ya Sekondari kwa wanafunzi viziwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kuandaa walimu wenye taaluma ya Elimu Maalum katika fani ya Uziwi na Lugha ya Alama kila mwaka. Aidha, Serikali inaendelea kupokea maoni ya wadau kuhusu uboreshaji wa mitaala ya elimu na mafunzo nchini ambapo suala la matumizi ya Lugha ya Alama katika mitaala hii litazingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: -

Je, ni Mikoa mingapi, Wilaya, Vijiji na Vitongoji wameunda Kamati za Watu wenye Ulemavu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, uundwaji wa Kamati za Watu Wenye Ulemavu katika Ngazi ya Mkoa, Wilaya, Vijiji na Vitongoji ni kwa mujibu wa Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na.9 ya mwaka 2010 kifungu cha 14(1) ambacho kimeelezea juu ya uundwaji wa Kamati za Watu Wenye Ulemavu katika ngazi ya Kijiji, Mtaa, Wilaya, Mkoa pamoja na majukumu ya kila Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, imetekeleza kwa kiwango kikubwa uundwaji wa Kamati hizo. Mchanganuo wa idadi ya Mikoa, Halmashauri na Vijiji/Mitaa ya Tanzania Bara iliyounda Kamati za Watu wenye Ulemavu ni kama ifuatavyo: -

(i) Mikoa yote 26;

(ii) Halmashauri zote 185;

(iii) Vijiji 7,483 kati ya 12,319; na

(iv) Mitaa 2,284 kati ya 4,263.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha na kufuatilia Vijiji na Mitaa yote inaunda Kamati za Watu Wenye Ulemavu, Serikali imeandaa mikakati mbalimbali ikiwemo kuingiza masuala ya Kamati za Watu Wenye Ulemavu kwenye Mwongozo Kabambe wa Upangaji wa Mipango na Bajeti ya Huduma za Ustawi wa Jamii kwenye Halmashauri (Council Comprehensive Social Welfare Operation Plan – CCSWOP) ambapo utekelezaji wake utaanza mwaka ujao wa fedha 2023/2024. Aidha, Serikali itaendelea kufuatilia Watendaji wa Vijiji au Mitaa ili kuhakikisha Kamati za Watu Wenye Ulemavu zinaanzishwa katika maeneo yao.
MHE. AGNES M. MARWA K.n.y. MHE. STELLA A. IKUPA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa kuna vyumba maalum kwa ajili ya kujifungulia wanawake wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshalitambua tatizo hilo na kwa muda mrefu sasa marekebisho yamekuwa yakifanyika kwenye miundombinu isiyo rafiki kwa wanawake wenye ulemavu na tayari kwenye ramani mpya za ujenzi wa vituo vya afya, hospitali, ununuzi wa vifaa tiba, mahitaji kwa watu wenye mahitaji maalum yamezingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: -

Je, lini Mfuko wa Taifa wa Watu wenye Ulemavu utaanza kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Taifa wa Watu Wenye Ulemavu umeanzishwa kwa mujibu wa Kifungu cha 57 cha Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010. Katika kutimiza azma ya Serikali ya uanzishwaji wa Mfuko huu, hatua mbalimbali zimeshachukuliwa na Serikali ikiwemo uandaaji wa Mwongozo wa Usimamizi, Uratibu na Uendeshaji wa Mfuko husika pamoja na kufunguliwa kwa akaunti ya mfuko.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kukamilika kwa hatua zote muhimu za mfuko kuanza kutekeleza majukumu yake, mfuko huu haujaanza kutoa huduma kutokana na maelekezo ya kuunganisha mifuko yote ya uwezeshaji wananchi kiuchumi yaliyotolewa mwaka 2020. Zoezi hili liliambatana na tathmini ya ufanisi wa utendaji wa mifuko. Aidha, tathimini hii itakapokamilika, wadau wote wataarifiwa juu ya uanzishwaji wa mifuko hiyo ukiwemo Mfuko huu wa Taifa wa Watu wenye Ulemavu, ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: -

Je, nini mpango wa Serikali kuingiza lugha ya alama kwenye mitaala ya elimu nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) K.n.y WAZIRI WA ELIMU SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inao mpango wa kuingiza lugha ya alama kwenye mitaala ya elimu nchini kwa lengo la kutatua changamoto ya mawasiliano kwa wanafunzi viziwi na katika jamii. Aidha, katika mchakato wa mapitio ya sera ya mitaala unaoendelea somo la Lugha ya Alama limependekezwa liwe la lazima kwa walimu wote tarajali katika vyuo vyote vya ualimu na vyuo vikuu nchini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwepo kwa mpango na mapendekezo hayo, tayari Serikali imeandaa na kusambaza kamusi ya lugha ya alama ya Tanzania ya kidijitali katika shule na vyuo vinavyopokea wanafunzi viziwi. Aidha, kozi ya lugha ya alama ya Tanzania inatolewa katika Chuo cha Ualimu Patandi na Kabanga na katika Vyuo Vikuu vya Dodoma, Dar es Salaam na Archbishop Mihayo University College Tabora kwa lengo la kumudu darasa jumuishi. Aidha, Serikali imeendelea kutoa mafunzo kwa walimu maalum na wasio wa elimu maalum 3,650 wa shule za msingi na sekondari kwa lengo la kuwajengea uwezo wa namna bora ya kuwafundisha na kuwahudumia wanafunzi viziwi ili kujenga jamii jumuishi ya viziwi shuleni.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-

Je, kuna mwongozo unaoruhusu watu wenye ulemavu mmoja mmoja kukopeshwa fedha za Halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa mtu mwenye ulemavu mmoja mmoja kuweza kupata mkopo ili kujikwamua kiuchumi na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya Taifa. Mwaka 2021 Serikali ilitoa mwongozo wa kumwezesha mtu mmoja mmoja kukopa kwa kufanya maboresho ya Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo kwa Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu za mwaka 2019 za Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, ambapo maboresho hayo yalihusisha kuongeza Kifungu kipya cha 6A(i) na (a) ambacho kwa sasa kinatoa fursa kwa mtu mmoja mmoja mwenye Ulemavu kukopa kutoka katika mikopo inayotolewa na Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge kuendelea kutoa elimu juu ya uwepo wa fursa hii kwa watu wenye ulemavu nchini kwa lengo la kujikwamua kiuchumi na kujiongezea kipato.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-

Je, Serikali inaonaje ikapunguza au kuondoa nauli kwenye vivuko vyote nchini kwa watu wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inafahamu kuwepo na Watu Wenye Ulemavu wa aina mbalimbali ambao wanatumia huduma za vivuko kote Nchini. Aidha, suala la kupunguza au kutolipa nauli kwenye vivuko halijatamkwa kwenye Sheria ya Leseni za Usafirishaji.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, suala la kupunguza au kuondoa nauli limekuwa likifanyika kwa Watu Wenye Ulemavu waliopo kwenye mazingira hatarishi katika vyombo mbalimbali ikiwemo usafiri wa vivuko. Hii imefanyika kupitia ofisi za Wakuu wa Wilaya kwa kushirikiana na Maafisa Ustawi wa Jamii katika Halmashauri husika.

Mheshimiwa Spika, aidha, nichukue nafasi hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuwaelimisha wananchi kuhusu utaratibu huu wa kupunguza au kuondoa nauli kwa Watu Wenye Ulemavu au wenye mahitaji maalum. Ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: -

Je, ni Halmashauri na Manispaa ngapi nchini zinatekeleza ununuzi na ugawaji wa mafuta ya ngozi kwa watu wenye ulemavu wa ngozi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, huduma kwa watu wenye ulemavu zimeendelea kuboreshwa kote nchini, ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022 jumla ya watu wenye ulemavu 138,468 kati yao wanawake 68,401 na wanaume 70,067 wametambuliwa. Aidha, katika kipindi hicho, watu wenye ulemavu wapatao 15,596 wamehudumiwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1.3.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuwakinga watu wenye ualbino dhidi ya maradhi ya ngozi kutokana na jua, kati ya mwaka 2020 hadi 2022 jumla ya Halmashauri 102 kwenye mikoa 20 imetekeleza ununuzi na ugawaji wa mafuta ya ngozi (sun-screen cream) kwa kushirikiana na wadau. Jumla ya wanufaika 3,389 walipata huduma hiyo. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI K.n.y MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-

Je, upi mkakati wa Serikali kufanya Marekebisho ya Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 ya Watu Wenye Ulemavu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nikushukuru na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii, lakini uniwie radhi kwamba nataka kutumia fursa hii kukupongeza sana, kwa kuwa Rais wa Mabunge Duniani, hii inadhihirisha uwezo mkubwa lakini weledi mkubwa ulionao katika kuongoza Bunge letu lakini pia kuaminika katika Dunia.

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kukupa fursa hiyo lakini zaidi pia kuweza kuwezesha jambo hili kufanikiwa. Haya ni mafanikio makubwa kwa nchi yetu na kwamba, imekuwa kielelezo wewe pamoja na Dkt. Samia Suluhu Hassan cha kufanya sasa leadership tourism katika nchi yetu ya Tanzania, wanaweza kuja kujifunza masuala ya uongozi kupitia Dkt. Samia Suluhu Hassan pia uongozi wako mzuri.

Mheshimiwa Spika, mimi najivunia kuwa wa kwanza kujibu swali leo mbele ya Rais wa Mabunge Duniani. Hili siyo jambo rahisi, najivunia sana hilo lakini pia ni Mbunge wa kipekee kwa sababu hata Waziri Mkuu wa Uingereza anatoka Jimboni kwangu, kwa hiyo ahsante kwa kuniongezea rekodi.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo naomba nijibu swali kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mkakati wa Serikali kwa sasa ni kufanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Maendeleo na Huduma kwa Watu wenye Ulemavu ya mwaka 2004 ambapo utekelezaji wake umeanza. Baada ya kukamilika kwa mapitio ya Sera ya mwaka 2004, ndipo hatua za Marekebisho ya Sheria ya Watu wenye Ulemavu (Na. 9) ya mwaka 2010 itaanza kwa kuzingatia mapungufu yatakayobainishwa katika tathmini ya utekelezaji wa Sera ya mwaka 2004. Ahsante.