Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ummy Ally Mwalimu (25 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nakushukuru, lakini nianze na kukishukuru Chama changu cha Mapinduzi na Wanawake wa UWT wa Mkoa wa Tanga kwa kunipa heshima hii ya kurudi tena katika Bunge hili.
Pia kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani yake kubwa sana kwangu, namwahidi tutachapa kazi, kama kauli mbiu ya Serikali inavyosema.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesikiliza michango, maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na tunawashukuru wote ambao wamechangia katika eneo hili. Lengo ni kutaka kuboresha utoaji wa huduma za afya, lakini pia kuhakikisha tunajenga jamii ya Watanzania inayojali na kuheshimu usawa wa jinsia, haki za wanawake, haki za watoto na haki za wazee. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na niwathibitishie katika hatua hii kwamba tutafanyia kazi maoni yenu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, nitajikita katika masuala makuu mawili ambayo yameongelewa sana na Waheshimiwa Wabunge wote. Kama walivyosema wenzangu, wakati wa kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Mpango wa Maendeleo wa 2016/2017 tutatoa mwelekeo wa vipaumbele vyetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala kubwa ambalo limechangiwa na Waheshimiwa Wabunge, lakini pia limejitokeza kwa sauti kubwa wakati wa Hotuba ya Mheshimiwa Rais ni suala la upatikanaji wa dawa katika vituo vya umma vya kutolea huduma za afya katika Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya na Hospitali za Rufaa za Mikoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwamba tumedhamiria kuhakikisha tunapunguza tatizo la ukosefu wa dawa katika hospitali zetu. Tayari tumeshaanza kuchukua hatua na kwa sasa hivi uwezo wetu wa kutoa dawa ni asilimia 70 na tunakusudia tufikie asilimia 95. Hii tutawezaje? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza dawa ambazo zinafika kwa wananchi, nyingi zinapotea mtaani katika mikono ambayo siyo salama. Kwa hiyo, kubwa ambalo tumelifanya na tutaendelea kulifanya ni kudhibiti upotevu wa dawa za Serikali na vifaa tiba. Sasa hivi tumeshaweka nembo katika dawa zote za Serikali ambazo ni muhimu. Asilimia 80 ya dawa za Serikali sasa hivi tayari zina nembo.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, tuendelee kuhamasisha wananchi wetu, watakapoona dawa ya Serikali ambayo ipo katika duka la dawa ambalo halistahili, watujulishe na wachukue hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ambalo tumelifanya ni kuimarisha mfumo wa usambazaji, ununuzi na uhifadhi wa dawa. Hili ambalo tumelifanya tumeshaagiza MSD kuhakikisha dawa hazishushwi katika kituo chohote cha afya cha Umma bila kuwepo kwa Kamati ya Afya ya Kituo husika.
Waheshimiwa Wabunge, sisi sote ni Madiwani, tuhakikishe Kamati za Afya za Zahanati, za Vitua vya Afya za Wilaya zinatimiza wajibu wao wa kuhakikisha tunadhibiti dawa na vifaa tiba vya Serikali.
Jambo lingine ambalo ningependa kulisisitiza, mpango wetu wa muda mrefu ni kuhakikisha tunanunua dawa kutoka kwa wazalishaji, badala ya kununua dawa kutoka kwa wafanyabiashara na hili linawezekana sana. Kauli mbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kwamba tunabana matumizi. Kwa hiyo, tunaamini tutakaponunua dawa kutoka kwa wazalishaji, tutaweza kupata dawa nyingi, lakini pia kwa bei nafuu na hivyo kuweza kutatua tatizo kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili, tutaongeza bajeti ya kununua dawa, vifaa na vifaa tiba. Waheshimiwa Wabunge, wameongelea suala la ukosefu wa X-Ray, Ultra-Sound, CT-Scan na MRI. Tayari tumeshachukua hatua, sasa hivi Muhimbili hamna shida tena katika vifaa hivyo vikubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mpango pale Wizarani wa kuhakikisha katika kila Hospitali ya Rufaa ya Mkoa tunaiwezesha katika eneo zima la uchunguzi, maana yake, ni vifaa vyote ambavyo vinahitajika katika kufanya uchunguzi. Tayari tumeshapeleka mapendekezo yetu kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, tuone ni jinsi gani tutaweza kusonga mbele.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa Mzungumzaji)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, duh!
Meshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni suala la miundombinu. Nikuhakikishie kwamba tutafanya kazi na wenzetu wa TAMISEMI kuhakikisha kwamba tunajenga zahanati katika kila kijiji, vituo vya afya katika kila Kata na Hospitali za Wilaya. Niwaambie Waheshimiwa Wabunge, hili kwa kweli, sisi la kwetu itakuwa tu ni kuweka vibali. Kwa hiyo, wale Wabunge wote ambao wamejenga vituo vya afya...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ummy, tafadhali weka nukta!
WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kusema, kama mwanamke, afya ya mama na mtoto ni kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Tano. Tutahakikisha tunapunguza vifo vya wanawake wajawazito na watoto chini ya miaka mitano. Hilo ni la kipaumbele, tutaongea kwenye Mpango wa Maendeleo. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijaalia afya njema. Pili, naishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii inayoongozwa na Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba, kwa maoni yao na ushauri mzuri kwa Wizara katika kuboresha utoaji wa huduma za afya nchini, pia katika kujenga jamii ya Watanzania inayojali na kuheshimu haki za wanawake, haki za wazee na haki za watoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru pia Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Dkt. Godwin Mollel kwa hotuba yake nzuri na niwashukuru Wabunge wote waliochangia hoja ambayo tumeianza toka jana. Jumla ya Wabunge 123 wamechangia hoja hii. Wabunge 63 wamechangia kwa maneno kwa kuzungumza na Wabunge 60 wamechangia kwa maandishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda na kwa mujibu wa Kanuni za Bunge nitashindwa kuwataja majina mmoja baada ya mmoja, lakini naomba Bunge tu litambue kwamba tunatambua michango yao, tunatambua ushauri wao na tupo tayari kusikiliza na kutekeleza ushauri mzuri waliotupatia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikiliza kwa makini taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge, nimesikiliza kwa makini taarifa ya Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na nimesikiliza kwa makini michango ya Wabunge waliyoitoa toka jana. Naomba nitoe maneno ya utangulizi matatu. Kwanza nilichojifunza kutokana na mijadala iliyokuwepo hapa toka jana ni kwamba afya haina itikadi, afya haina vyama, afya haina rangi, afya haina kabila. Tumepata michango mizuri sana, watu wameweka ushabiki wa vyama pembeni, wamejikita kuchangia kwenye hoja ambayo iko hapa mezani, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge, tunathamini sana michango yenu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka kulianza la jumla ni kwamba, kutokana na mijadala toka jana, jambo ambalo limejitokeza wazi hakuna viwanda bila afya, hakuna ulinzi bila afya, hakuna kilimo bila afya, hakuna elimu bila afya na Mheshimiwa Mwigulu rafiki yangu anasema ukitaka mali utaipata shambani, lakini lazima tu-qualify huo msemo ukitaka mali utaipata shambani endapo utakuwa na afya bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu la jumla ambalo nataka kulisema hapa mbele ya Bunge lako Tukufu ni kwamba, tunatambua jukumu kubwa ambalo mimi na wenzangu tumekabidhiwa katika kuboresha utoaji wa huduma za afya nchini. Jukumu hili ni kubwa lakini nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba, uwezo, dhamira na nguvu ya kupambana, kuhakikisha tunaboresha huduma za afya nchini tunao, pia katika kuhakikisha tunajenga jamii ya Kitanzania, inayowajali na kuwaheshimu wasichana na wanawake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno hayo ya utangulizi, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kutoa ufafanuzi na Waheshimiwa Mawaziri pacha wangu Angellah Kairuki pia Naibu Waziri wa TAMISEMI na Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda, naomba nijikite kwenye hoja kubwa ambazo zimetolewa na Kamati na Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani. Naomba nisijikite kwenye hoja moja moja za Wabunge maana nina page takribani 175, nikisema namjibu kila Mbunge mmoja kwa kweli nitashindwa kumaliza. Nitajikita katika mambo makubwa matano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo limeongelewa ni suala la upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya sekta ya afya, Mheshimiwa Naibu Waziri amesaidia kufafanua, lakini nataka kujikita katika rasilimali fedha ambazo zinatoka katika chanzo cha Serikali Kikuu ambacho ni Hazina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano inatoa kipaumbele kwa sekta ya afya kwa sababu tukiangalia mwenendo wa mapato wa fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya sekta ya afya kwa Wizara yangu Fungu 52 na kwa ajili ya TAMISEMi utaona kwamba kumekuwa na ongezeko la bajeti ya fedha kwa ajili ya sekta ya afya. Kuanzia mwaka 2008 mpaka 2009, bajeti ilikuwa bilioni 769, mwaka 2014/2015, bajeti ya sekta ya afya ilikuwa trilioni 1.5 na kwa mwaka 2015/2016 bajeti ya sekta ya afya ilikuwa trilioni 1.8, mwaka huu wa fedha sekta ya afya imepatiwa maombi au imetengewa na Hazina bajeti ya shilingi trilioni 1.9. Kwa hiyo, kaka yangu Mheshimiwa Zitto nataka kuliweka wazi, ukichukua bajeti yote ya Serikali ya trilioni 29 na ukigawanya kwa 1.9, sekta ya afya siyo chini ya asilimia nne tuko kwenye asilimia saba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili kwa kweli tunatambua kwamba hatutaweza ku-finance hii sekta kwa asilimia mia moja kutoka Hazina. Naibu Waziri amelieleza vizuri, tunajikita katika kutafuta vyanzo vingine vya ku-finance na kuweza kusimamia sekta hii ya afya. Kubwa ambalo tunategemea kwamba tutapata fedha ni kwa kupitia huduma kwa kupanua wigo wa Mfuko wa Bima ya Afya lazima tuhakikishe Watanzania wengi wanakuwa wanachama wa Bima ya Afya kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri. Mwezi wa Septemba nitakuja mbele ya Bunge lako Tukufu kuwasilisha Muswada ambao utawataka Watanzania wote kuwa na Bima ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie kuhusu utegemezi wa bajeti ya afya kwa wadau wa maendeleo, kwamba fedha za nje zimepungua nataka kuwathibitishia dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kuhakikisha tunatumia fedha zetu za ndani kwa ajili ya kutatua changamoto zetu. Hili nataka kulionesha kwamba kutokana na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kutumia fedha zetu za ndani badala ya kutegemea wafadhili wa nchi za nje, tumeongeza bajeti ya vyanzo vya ndani kutoka bilioni 66 mwaka 2015/2016, sasa hivi tuna bilioni 320. Ni fedha zetu wenyewe Watanzania ambazo tutaweza kutumia kwa ajili ya kutatua changamoto mbalimbali za sekta ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite katika suala la pili ambalo limetolewa maoni na Waheshimiwa Wabunge wengi nalo ni suala la upatikanaji wa dawa. Nikiri kwamba tunazo changamoto katika upatikanaji wa dawa, lakini binafsi nauona mwanga baada ya kutoka katika shimo kubwa. Nauona mwanga kwa sababu bajeti ya kwanza ya dawa ya Serikali ya Awamu ya Tano imeongezeka kama tulivyoonesha, kutoka shilingi bilioni 66 lakini sasa hivi bajeti yetu ni shilingi bilioni 251 na hii 251 tumeiweka kwamba tutalipa deni la MSD ambalo ni takribani shilingi bilioni 85 na hela zinazobaki tutazitumia kwa ajili ya kununua dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukiniuliza bajeti yangu ya kwanza ya afya, kipaumbele chake ni nini? Nitajibu mbele ya Bunge lako Tukufu na napenda kuwathibitishia Watanzania kwamba, bajeti hii ni bajeti ya dawa kwa sababu tutaweza kulipa deni la MSD zaidi ya bilioni 85.2, pia tumeweka fedha kwa ajili ya kununua dawa. Tumefanya haya makisio ni shilingi ngapi tunahitaji kwa ajili ya kununua dawa kwa mwezi? Kwa mwezi tunahitaji takribani bilioni 21, kwa hiyo kwa mwaka tunahitaji bilioni 252 na Mheshimiwa Rais ametupa maombi yetu kwa asilimia mia moja yamepitishwa, ndiyo tutalipa deni, lakini ndiyo fedha ya dawa, kwa hiyo tutaweza kulipa deni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme Watanzania wajue kwamba, maneno ya Rais kwamba, tutatatua changamoto ya upatikanaji wa dawa hayakuwa maneno ya kuomba kura, yalikuwa ni maneno ya dhati na ndiyo maana dhamira yake hii ameionesha katika bajeti yake ya kwanza ya dawa. Ongezeko la dawa ni asilimia 810 ukilinganisha na bajeti ya dawa ya mwaka 2015/2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zimesemwa changamoto mbalimbali kuhusu usambazaji na uhifadhi wa dawa. Changamoto zipo lakini tutaboresha mfumo mzima wa usambazaji ikiwemo ununuzi wa dawa kuhakikisha kwamba dawa zinafika katika vituo vyetu vyote vya afya kupitia bohari ya dawa. Tumeshatoa maelekezo pia kuhakikisha kwamba dawa lazima zifike, tatizo kubwa dawa zilikuwa zinachelewa kwa sababu MSD ilikuwa haina mtaji, lakini kama tutaweza sasa kupata hii fedha, tukawalipa deni, MSD wakawa na fedha ya ziada ya kununua dawa naamini dawa zitafika kwa Watanzania, dawa zitafika katika zahanati zetu na zitafika katika vituo vya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe angalizo kwa sababu Waheshimiwa Wabunge ni Madiwani, ni lazima na sisi tuzihimize Halmashauri zetu kuleta mapema maoteo yao ya dawa badala tu ya kushtukiza muda umefika ndiyo wanaleta maoteo yao ya dawa. Pili hatuwezi kutegemea fedha hizi za dawa za kutoka Serikali Kuu. Tutaendelea kuhimiza na kuhamasisha Halmashauri zitumie mapato yao ya ndani kwa ajili ya kununua dawa, vifaa na vifaa tiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetoa mfano wa baadhi ya hospitali kabla ya kudhibiti mifumo ya ukusanyaji mapato walikuwa wanapata fedha ndogo, kwa mfano hospitali ya rufaa ya Kanda ya Mbeya walikuwa wanakusanya milioni 50 mpaka milioni 60 kwa mwezi, sasa hivi wanakusanya zaidi ya milioni 500. Kwa hiyo, kadri kituo cha afya kinavyokusanya fedha za mapato ya Bima ya Afya au ya papo kwa papo maana yake pia wataweza kujenga uwezo wao wa ndani wa kuhakikisha kwamba wananunua dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kwenda eneo la tatu nimezungumza suala la MSD kufungua maduka ya dawa. Tunataka kusema kwamba kwa sasa hivi tunataka kujikita katika hospitali za Rufaa za Kanda, hospitali kuu hizi za Kitaifa na hospitali za Rufaa za Mikoa. Nimeyasikia maombi ya akina Mheshimiwa Shabiby, Mheshimiwa William Ngeleja na Mheshimiwa Anna Lupembe kwamba twende sasa katika ngazi ya Wilaya na Wabunge wote ambao sikuweza kuwataja. Kwa hiyo, tunaomba sasa hivi kwa mwaka huu wa fedha mtuache kwanza tuishie katika ngazi ya hospitali za Rufaa za Mikoa, lakini lengo letu ni kuhakikisha kwa kweli tunapunguza changamoto zinazojitokeza katika upatikanaji wa dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja katika eneo hili ni kwamba, Serikali ya Awamu ya Tano imefanya maamuzi magumu kwamba dawa karibu zote sasa hivi tutanunua kutoka kwa wazalishaji badala ya kununua kutoka kwa wafanyabiashara Dar es Salaam. Tunapingwa sana na wafanyabiashara. Kwa hiyo, hii itatusaidia kuhakikisha kwamba tunanunua dawa moja kwa moja na tayari tumeshapeleka mapendekezo kwa Waziri wa Fedha kuhakikisha kwamba Sheria ya Manunuzi pia inaondoa dawa katika bidhaa ambayo itafuata taratibu zile ambazo kidogo ni ndefu za kununua dawa na vifaa na vifaa tiba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna eneo kubwa ambalo limeongelewa na Waheshimiwa Wabunge takribani wote ni vifo vya mama na mtoto na mimi ni mama wa mabinti warembo wawili na mume wangu leo yuko hapa. Kwa hiyo, kama mwanamke naguswa na suala la vifo vitokanavyo na uzazi, lakini niweke wazi kwamba kwanza sitaki kubishana na Bunge lako Tukufu kwamba vifo hivi ni 42 kwa siku au ni vifo 22 kwa siku. Ninachotaka kusema ni msimamo wetu Serikali, msimamo wa Wizara, kwa mujibu wa taarifa ya Umoja wa Mataifa ambayo imetolewa mwaka 2015 na ambayo ndiyo tunaitumia, kwa mujibu wa taarifa hii vifo ni 22 kwa siku na siyo vifo 42 kwa siku. Hii haitupi sisi sababu ya kutochukua hatua, haitupi sisi sababu ya kuhakikisha hawa wanawake 42 na wenyewe tunawahakikishia usalama wao na usalama wa vichanga vyao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya utafiti na kugundua sababu zinazopelekea vifo vya akinamama wajawazito. Sababu ya kwanza ni kutokwa na damu nyingi ambapo ni takriban asilimia 19, pia kuna kifafa cha mimba, kuna masuala ya uzazi pingamizi lakini kuna uambukizi na sababu nyingine ikiwemo ukosefu wa damu, malaria na maambuzi ya VVU- UKIMWI. Kwa hiyo, Bunge lako Tukufu pamoja na Kamati wakiwemo Waheshimiwa Wabunge wametaka kujua tumejipangaje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo tutalifanya ni kuhakikisha tunapandisha hadhi vituo vya afya ili viweze pia kufanya upasuaji wa kutoa mtoto. Tukifanya hivi maana yake tutapunguza vifo kwa takribani asilimia11 na la pili ambalo tutalifanya ni kuhakikisha kwamba tunahakikisha upatikanaji wa damu salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala hili nipongeze vyama vyote, chama changu Chama cha Mapinduzi kupitia Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu Hassan wamejitolea kukusanya damu lakini pia tumeona wenzetu wa Chama cha CHADEMA na wenyewe wakijitolea kukusanya damu. Ndiyo maana tunasema afya haina itikadi, afya haina vyama. Niko tayari kuambatana na kushirikiana na vyama vyote endapo tu tutaweza kupata damu salama ili tuweze kuokoa akinamama wajawazito. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutahakikisha pia tunaanzisha benki za damu salama katika mikoa na kanda mbalimbali na tayari nimeshatoa maelekezo na naomba nitoe maelekezo kwa Waganga Wakuu wa Mikoa na Waganga Wakuu wa Wilaya, kuhakikisha angalau kila mwezi wanakuwa na mpango wa kuchangia damu salama kwa wiki. Tukifanya hivi tutaweza kuhakikisha tunaokoa maisha ya akinamama wajawazito. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo tutalifanya ni kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi ya wanawake wajawazito ambao wanahudhuria kliniki na kujifungua katika vituo vya afya. Ukiangalia takwimu sasa hivi ni takriban wanawake asilimia 51 ndiyo wanajifungua katika vituo vya afya. Tutaendelea kufanya mikakati na programu mbalimbali za kuhamasisha wanawake kujifungua katika vituo vya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu Mheshimiwa Hussein Bashe, Mheshimiwa Bonnah Kaluwa, Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mheshimiwa Abdallah Mtulia na Mheshimiwa Zuberi Kuchauka wameongelea kwa uchungu suala la vifaa vya kujifungulia wanawake, tena kaka yangu Mheshimiwa Zuberi ndiyo ametoa mfano mbaya. Mwanamke anakwenda na beseni utasema anakwenda kufunga harusi! Kwa sababu na mimi nimepita labour mara mbili, nimeshafanya maamuzi katika bajeti hii, tutatoa vifaa bure vya kujifungulia kwa wanawake wajawazito na tutaanza na wanawake laki tano. Tutagawa kutokana na uwiano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Liwale wanazalisha kwa mwaka wanawake 80, kwa hiyo tutakupa asilimia 25 ya wanawake hawa, lakini lengo letu ni wanawake wote wanaokwenda kujifungua wapate vifaa hivi bure, badala ya kufikiria pamba, mkasi au gloves, tunataka wanawake wafikirie jambo moja tu, la kusukuma kutoa mtoto, hili linawezekana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutahakikisha pia tunahamasisha wanawake kutumia njia za uzazi wa mpango, pia kuongeza ushiriki wa jamii katika masuala haya ya uzazi salama. Jana nilitoa mfano wa Kijiji cha Uturo ambacho tangu mwaka 1998 hawana vifo vitokanavyo na uzazi kwa sababu tu wao jamii imeamua kushirikiana nao na wameweza kupunguza vifo hivi na kwa kuwatumia wahudumu wa afya ngazi ya jamii ambapo tunawaita Community Health Workers. Katika bajeti hii tutaajiri wahudumu wa afya ngazi ya jamii ili waweze kuhamasisha na kutoa elimu ya afya ile ya awali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumezungumzwa suala la upatikanaji wa ambulance nalo linasaidia kwa kiasi fulani kuokoa vifo vya akinamama wajawazito. Nataka niseme bajeti hii haijapanga kununua ambulance hata moja kwa hiyo amesema vizuri Mheshimiwa Jaffo, Naibu Waziri wa TAMISEMI, hili ni jukumu la Halmashauri husika. Natoa changamoto kwa Wabunge Wanawake na Madiwani Wanawake wa Tanzania, hivi mko wapi wakati Halmashauri inapanga vipaumbele, hawapangi vipaumbele vya uzazi salama? Lazima hili tulibebe, Wabunge wanawake tuungane, Madiwani wote wanawake lazima washike hatamu katika kuhakikisha kwamba Halmashauri zinaweka vipaumbele katika uzazi salama ikiwemo kujenga vituo vya afya, ikiwemo pia kununua haya magari ya wagonjwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowashukuru Waheshimiwa Wabunge. Najua Wabunge wengi wamenunua magari ya wagonjwa (ambulance), Wabunge wengi wamenunua mashuka, vifaa na vitanda vya kujifungulia. Tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na nasema mnawatendea haki wapiga kura wenu kwa sababu asilimia 51 ya wapiga kura wenu ni wanawake. Kwa hiyo, ni matarajio yangu kuona Mfuko wa Jimbo ukielekezwa kwa kiasi kikubwa kutatua changamoto zinazowakabili wanawake ikiwemo suala la uzazi salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana Wabunge wanawake pia naelewa kwa nini wanaomba na wenyewe wapewe Mfuko wa Jimbo ili wakaweze kutatua changamoto zinazowakabili wanawake katika Majimbo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nizungumzie suala la huduma za uzazi wa mpango, ni kweli tunakubali kwamba Tanzania ni mojawapo ya nchi yenye ongezeko kubwa la watu takriban kwa asilimia 3.1 kwa mwaka. Ili kuonesha kwamba Awamu ya Tano imedhamiria kutatua changamoto hii. Tumeweza kubajeti fedha ingawa siyo fedha kubwa, lakini kwa mara ya kwanza tumeweka bilioni tano za ndani kwa ajili ya kufanyia kazi ya kutatua changamoto zinazohusika na huduma za uzazi wa mpango. Tulikuwa tunategemea wafadhili wa nje lakini ili kuonesha dhamira yetu ya wazi tumeamua kutenga fedha za ndani kwa ajili ya uzazi wa mpango, of course na wadau wetu wa maendeleo wametutengea bilioni 12.8 kwa ajili ya uzazi wa mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kwamba wanawake wengi wanataka kutumia huduma za uzazi wa mpango na hatujaweza kuwafikia kwa sababu sasa hivi kwa mujibu wa TDHS ya mwaka 2010, takriban wanawake asilimia 20 tu ndiyo wanatumia matumizi haya ya njia za kisasa za uzazi wa mpango, lengo letu ni kuhakikisha tunapokwenda mwaka 2020 tufikie wanawake asilimia 60.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda pia naomba nimalize kwa kusema katika suala la vifo vya akinamama wajawazito ni eneo la kipaumbele changu, hivyo ni kipaumbele cha Wizara na kipaumbele cha Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan. Tunaamini kwamba wanawake wenzetu hatutawaangusha na tutaleta mabadiliko makubwa katika kuboresha huduma ya afya ya uzazi na mtoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, limeongelewa suala la matibabu kwa wazee, ninayo Sera ya Afya ya mwaka 2007. Kwa mujibu wa Sera ya Afya ambapo mimi nimepewa dhamana ya kuisimamia, bado wazee kuanzia miaka 60 wanatakiwa kupata matibabu bure, wajawazito wanatakiwa kupata matibabu bure na watoto chini ya umri wa miaka mitano wanatakiwa kupata matibabu bure. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejaribu kuongea na wenzangu na kaka yangu Mheshimiwa Bashe ali-propose kwamba tuwakatie Bima ya Afya wanawake wajawazito ambapo kwa mujibu wa takwimu zetu deliveries kwa mwaka ni kama milioni 1.2 mpaka milioni 1.5. Tumepiga mahesabu, milioni 1.5 ukizidisha mara 50,400 ni takriban bilioni 76, sitaki kudanganya Wabunge, sitaki kudanganya Bunge lako kwamba tutakuwa nazo bilioni 76, lakini tutakachofanya ni kuona ni jinsi gani Mfuko wa Bima ya Afya na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii inachukua hatua, inaongeza jitihada katika kuhakikisha sera za Serikali zinatekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa wazee tutahakikisha kwamba madirisha haya ya wazee katika hospitali zetu yanafanya kazi na kwa mujibu wa sera ni kwamba mzee anatakiwa kupata huduma za ushauri wa Daktari (consultation) iwe ni bure. Vipimo mzee anatakiwa kuwa bure, pale ambapo labda dawa hakuna ndipo mzee ataambiwa akanunue dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie Bunge hili kuwataka Waganga Wakuu wa Mikoa wote, Waganga Wakuu wa Wilaya wote na Wakuu wa hospitali za umma wote, kuhakikisha kwamba wanatoa huduma za matibabu bure kwa wazee na tutahakikisha kwamba hiyo changamoto ya dawa kwa wazee tunaitatua. Nimeshamuagiza Mfamasia Mkuu wa Serikali kwamba katika kila ile bajeti ya dawa, basi tutenge asilimia ya fedha kwa ajili ya kununua dawa kama nne au tatu muhimu kwa ajili ya matibabu ya wazee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafurahi kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba, jambo hili wenzangu wamelikubali, kwa hiyo, tutaelekeza kwamba kwa mfano Halmashauri inanunua dozi laki moja za antibiotic, wazee ni asilimia 5.6, sioni ni kwa nini tushindwe kuwahudumia wazee wetu. Katika kila Watanzania 100 maana yake utakuwa na wazee sita. Hili jambo linawezekana kabisa. Kwa hiyo, tutahakikisha katika kila dawa tunatenga dawa kama tatu au nne ambazo zinagusa magonjwa ya wazee mara kwa mara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Magu, wao hawajatenga tu dirisha kwa ajili ya wazee, lakini wameweka sehemu maalum kwa ajii ya kutoa matibabu kwa wazee. Mzee akienda pale anapata vipimo, anapata dawa, anamwona Daktari! Kwa hiyo, nitoe changamoto kwa Waheshimiwa Wabunge, wazee ni hazina na kama kampeni yetu inavyosema, “mzee alikuwa kama wewe na wewe utakuwa kama yeye, tutoe kipaumbele cha huduma kwa wazee”. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize suala la upatikanaji wa huduma za afya. Waheshimiwa Wabunge wameongea, tangu jana. Nashukuru sana Mheshimiwa Joseph Mbilinyi (Sugu) kidogo alitusaidia, kwa sababu Wabunge tangu jana wameongea kuhusu zahanati, wameongea kuhusu vituo vya afya, wameongea kuhusu hospitali za Wilaya. Hatukatai kwamba Sera ya Afya iko chini ya usimamizi wa Wizara ya Afya, lakini anayetakiwa kuweka hii miundombinu ni wenzetu wa TAMISEMI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu nimeona upatikanaji wa huduma za afya katika ngazi ya chini unahusiana moja kwa moja na kupunguza vifo vya akinamama wajawazito na watoto, tumeshakaa na mwenzangu Mheshimiwa George Simbachawene na kuona kwamba, ni lazima baada ya bajeti yangu, kesho, wataalam wangu watatu watakaa pamoja na wataalam watatu wa Mheshimiwa Simbachawene na watu wa Fedha, tuoneshe ni jinsi gani sasa tutajenga vituo vya afya, tutajenga hospitali za wilaya na hospitali za mikoa katika mikoa ambayo haina huduma hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge. Wizara ya Afya kazi kubwa ambayo ilifanya ni kuhakikisha ujenzi wa miundombinu umeingia katika Mpango wa Maendeleo wa Pili wa mwaka 2016 - 2021 na pesa zimetengwa. Kwa hiyo, tutaonesha katika kila mwaka tutajenga vituo vya afya vingapi na tutajenga hospitali za Wilaya ngapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge, naamini kwa boss wangu Mheshimiwa Rais, Dkt, John Pombe Magufuli ambaye anataka kuona mambo tangible, tutaweza kujenga vituo vya afya katika kata zetu, katika wilaya zetu. Nataka kuwathibitishia, maneno yaliyokuwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi yatasimama na tutaonesha matokeo yake. Mwaka 2020 tutakapokuja kwa Watanzania tuwaeleze tumejenga vituo vya afya vingapi na hospitali za wilaya ngapi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sijui nina muda kiasi gani niende kwenye eneo la jinsia. Sitawatendea haki wanawake wenzangu, watoto kama sitagusa suala la usawa wa jinsia na uwezeshwaji wa wanawake. Nataka kujikita katika mambo makubwa mawili. Jambo la kwanza ambalo limechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wengi akiwemo dada yangu Mheshimiwa Faida Bakar, Mheshimiwa Aida Khenani na Mheshimiwa Anna Lupembe kwamba Benki ya Wanawake tunataka kuiona ikienda katika mikoa, katika wilaya na katika kata mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuwathibitishia kwamba katika mwaka huu wa fedha tutafungua vituo vitatu vya Benki ya Wanawake katika mikoa mitatu. Pia nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba tutaanza kutoa mikopo yenye riba nafuu kati ya riba ya asilimia 10 mpaka asilimia 12 ili Benki ya Wanawake iweze kukidhi matarajio ya kuanzishwa kwake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo pia tutalifanya kupitia Benki hii ya Wanawake ni kutoa mikopo midogo ya kuanzia laki mbili mpaka milioni moja bila kuwataka wanawake watoe dhamana ya hati ya kiwanja, hati ya nyumba au wengine wanatoa fenicha, wengine wanaambiwa walete sijui mikufu yao, hatutafanya hivyo. Tunataka kuonesha ni kiasi gani tumedhamiria kuwakomboa wanawake wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kuhusu haki za mtoto na hapa niwapongeze wadogo zangu watatu, Mheshimiwa Upendo Peneza, Mheshimiwa Halima Bulembo na Mheshimiwa Maria Kangoye, wameonesha ni jinsi gani wanaguswa na tatizo na changamoto zinazowakumba wasichana wenzao. Pia Mwalimu Kasuku S. Bilago na Mheshimiwa Mama Margaret Sitta wamegusia kwa kiasi fulani haki ya mtoto wa kike kupata elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuwathibitishia Watanzania, Serikali ya Awamu ya Tano inaamini kwamba, maendeleo ya kweli na endelevu ya Tanzania hayataweza kupatikana iwapo asilimia kubwa ya wanawake hawatakuwa na elimu. Mimi ni muumini, mbeleko ya kweli ya mwanamke na mtoto wa kike ni elimu, habebwi na kitu kingine chochote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo takwimu ambazo zinaonesha kwamba, kwa kila mwaka mmoja ambao mtoto wa kike anapata elimu, unamkinga na maambuzi ya UKIMWI mara saba, lakini katika kila mwaka mmoja ambao mtoto wa kike anapata elimu unamuepusha na vifo vya uzazi. Kwa hiyo, tutahakikisha kwamba tunatatua changamoto zinazomkabili mtoto wa kike katika kupata elimu ikiwemo kupata zana za kujisitiri ili kuhakikisha kwamba watoto wetu wanasoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muda umekwisha, lakini katika suala la ukeketaji, ukatili dhidi ya wanawake na wasichana na wanaume pia, dawati letu lile linaitwa Dawati la Jinsia, haliitwi dawati la wanawake, kwa hiyo wanaume ambao mnapata vipigo ndugu zangu msione aibu, nendeni mkaripoti kwenye Dawati la Jinsia ili muweze kupata haki zenu. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la mwisho la maendeleo ya jamii, Waheshimiwa Wabunge wamependekeza kwamba Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi tuvihamishe viende VETA. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba, tayari Mheshimiwa Rais kwa mujibu wa mamlaka aliyopewa, amehamisha Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi kwenda Wizara ya Elimu ili viweze kutoa mafunzo ya VETA. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kumshukuru tena Mheshimiwa Rais kwa kuniamini, pia nakishukuru sana chama changu Chama cha Mapinduzi na wanawake wa Mkoa wa Tanga kwa kunirudisha Bungeni. Nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri, Watendaji wote wa Wizara, Katibu Mkuu Dkt. Mpoki, Katibu Mkuu Mama Sihaba Mkinga na Waheshimiwa Mawaziri wote, hasa Mheshimiwa Angellah Kairuki na Mheshimiwa George Simbachawene ambao wananipa ushirikiano mkubwa katika utendaji wa kazi zangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tena, jana nilimshukuru mume wangu lakini hakuwepo, namshukuru sana, sana kwa uvumilivu wake na kwa moyo wake wa kunishauri na kunitetea. Nakushukuru sana Mume wangu Paschal, Mwenyezi Mungu akubariki, Mwenyezi Mungu akuzidishie heri. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami jianze kwa kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Taarifa yao, lakini nawashukuru kwa ushauri na maoni ambayo wamekuwa wakitupatia mara kwa mara katika kuboresha utendaji wa Wizara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua hii niseme kwamba Wizara yangu inapokea maoni na ushauri wa Kamati kama walivyoyawasilisha hapa na ninaahidi kwamba tutayafanyia kazi masuala yote waliyoyabainisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, napenda kutoa ufafanuzi katika masuala makuu matatu kama muda utatosha na suala la kwanza ni kuhusu hali ya upatikanaji wa dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ya upatikanaji wa dawa nchini ilikuwa inasababishwa na upatikanaji wa fedha, lakini hivi ninavyosema tumetoka katika kutaja bajeti ya Afya ya shilingi bilioni 251 na kusema pesa ambazo Wizara ya Afya imepokea; mpaka sasa hivi tumepokea shilingi bilioni 91 kwa ajili ya kununua dawa, vifaa na vifaa tiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia mwaka 2016 MSD ilipokea shilingi bilioni 24 tu kwa mwaka mzima kwa ajili ya kununua dawa. Sasa hivi kila mwezi Wizara ya Fedha inatuletea shilingi bilioni 20. Tumetoka kwenye kupokea shilingi bilioni mbili kila mwezi tunapokea shilingi bilioni 20 kila mwezi kwa ajili ya dawa. Kwa hiyo, baada ya kuwa tunapata fedha, hali ya dawa kwa kiasi kikubwa inazidi kuimarika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niseme tunapimaje upatikanaji wa dawa? Tunaangalia upatikanaji wa dawa katika Bohari Kuu ya Dawa. Hivi sasa MSD ana aina za dawa 105 kati ya dawa 135 muhimu za kuokoa maisha. Hii ni sawa na 78%. Nakiri kwamba sasa hivi kazi inayoendelea ni kuhakikisha dawa hizi sasa zinashuka katika zahanati zetu na vituo vya afya.
Waheshimiwa Wabunge, nimewaandikia barua na kesho mtaipata kuainisha mchanganuo wa kila fedha ya dawa ambayo tumebajeti katika Halmashauri yako ili uweze kupima. Kubwa tunawaomba msimamie matumizi ya fedha za dawa na matumizi ya dawa. Hali ya upatikanaji wa dawa kama wote hatutaimarisha Kamati za Vituo, basi hatutaweza kuwa na upatikanaji wa dawa hasa katika ngazi za chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nitoe angalizo, hatuwezi kuwa na upatikanaji wa dawa kwa asilimia 100 kwa sababu ya ongezeko la watu kila siku, ongezeko la magonjwa na vituo. Kwa hiyo, kubwa ambalo Wizara ya Afya tunalifanya sasa hivi ni kujikita kwenye kinga badala ya tiba. Maana inakuwa ni Taifa la kujikita kwenye tiba badala ya kinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ambayo tumeibaini ni MSD anabajeti fedha ya kununua dawa kutoka kwenye Fungu 52 - Wizara ya Afya, lakini kuna fedha za Mfuko wa Pamoja wa Afya, kuna vyanzo vya makusanyo tumeomba wenzetu wa TAMISEMI, maana MSD ananunua dawa za wateja za shilingi bilioni 70, lakini wateja wake wana fedha za kununua dawa za shilingi bilioni 300. Kwa hiyo, haiwezekani MSD kuweza kutosheleza soko lake. Nawaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba tutafanyia kazi suala hili la kuhakikisha dawa zinafika kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwamba MSD ipewe fungu, tulipokea ushauri wa Kamati na tukamwandikia Waziri anayehusika na masuala ya Utumishi na Utawala Bora kwa sababu wao ndio wanatoa Vote. Wakatushauri tuombe line item. Sasa hivi tuna line item katika Bajeti ya Wizara ya Afya kwa ajili ya MSD.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Halmashauri ambazo zinadaiwa fedha na MSD ziruhusiwe zilipe kidogo kidogo; tumepokea pia ushauri wa Kamati. Sasa hivi katika ile fedha ambayo tunaingiza katika bajeti ya Halmshauri, tunakata asilimia 25 tu, asilimia 75 tunawapa kwa ajili ya kusaidia upatikanaji wa dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu deni la MSD, mpaka sasa hivi tumelipa shilingi bilioni 11, lakini tumeona chanzo kinachofanya deni hili likawa kubwa ni tozo. Kwa hiyo, tayari tumewaelekeza tupitie tozo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya. Kamati inashauri kwamba i-cover magonjwa yote. Nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba kuanzia mwezi Septemba tumeingiza kitita cha huduma za upasuaji wa moyo na matibabu mengine ya hali ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu NHIF kusimamia kuweza kutumika Bima zao mpaka nchi za Afrika Mashariki, sheria iliyoanzisha NHIF inaruhusu NHIF kufanya kazi ndani ya nchi. Tumepokea ushauri na tutaleta. Waheshimiwa Wabunge ni mapendekezo yenu, tutayaleta hapa ili NHIF itumike ndani ya nchi za Afrika Mashariki, nasi tuko tayari na ninaamini kwamba Muswada huu mtaweza kuupitisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti,…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize neno moja tu. Kuhusu uzazi wa mpango, nakubaliana na ushauri wa Kamati kwamba ni changamoto kubwa, Waheshimiwa Wabunge mtuunge mkono. Ni asilimia 32 tu ya wanawake wanaotumia uzazi wa mpango. Lengo letu ni kuhakikisha huduma hizi zinapatikana mitaani badala tu ya kwenye vituo vya afya na hospitali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uzazi salama ni kipaumbele chetu. Nawathibitishia Waheshimiwa Wabunge, nikiwa Waziri mwanamke na mama wa watoto wawili, tutasaidiana kupunguza vifo vya akina mama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na ahsante kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kuishukuru sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii kwa jinsi ambavyo wameandika ripoti yao vizuri na ushirikiano wanaotupa katika kufanya na kutimiza majukumu yetu. Niwahakikishie kwamba mapendekezo yao mazuri sana waliyoyatoa kwenye ripoti yao tutayafanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Mheshimiwa Kadutu kuwapongeza sana Serengeti Boys kwa mafanikio makubwa waliyoyapata na kuipa heshima nchi yetu kwa kufanikiwa kwenda kwenye fainali za Afrika kwa vijana chini ya umri wa miaka 17. Niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba hata kufika pale walipofika kuna mkono mkubwa sana wa Serikali. Wakati mwingine siyo kila jambo unalisema hadharani, lakini ni hakika kwamba mkono wa Serikali umesaidia wao kucheza na kufika pale walipofika, lakini pia kusukuma rufaa yao mpaka wakapata kushinda na kwenda kwenye fainali za mashindano haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie Watanzania kwa pamoja, bila kujali tofauti zetu tuungane kwa pamoja, tuwatie moyo vijana hawa na kuwasaidia. Tunaamini watafanya vizuri kwenye mashindano haya na bila shaka tunaweza tukarudi na kombe. Wakifika nusu fainali, basi tuna uhakika wa kwenda kwenye Kombe la Dunia la Vijana chini ya miaka 17. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maelezo mazuri ya Kamati na wameainisha humu changamoto ambazo zinaikabili sekta ya michezo, niseme tu moja ya eneo kubwa ambalo linatusumbua sana ni namna ya ku-finance michezo katika nchi yetu. Niahidi katika Bunge hili kwamba tutaleta hapa Bungeni mpango mahsusi wa ku-finance michezo katika nchi yetu na hili litakuwa jibu la tatizo hili la kuendelea kwa michezo katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapitia Sera ya Michezo kama walivyoeleza katika taarifa yao na baada ya muda sera hii itakamilika, iko katika michakato ya mwisho. Ikikamilika, tutaleta sheria na kanuni zake hapa na bila shaka itasaidia sana katika ukuaji wa sekta ya michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja la mwisho ambalo nilipenda nilizungumzie ni suala la usikivu na utendaji kazi wa Shirika la Utangazaji la Taifa. Ni kweli kama ilivyooneshwa kwenye ripoti ya Kamati, Wilaya 81 za nchi yetu TBC haisikiki kabisa. Waheshimiwa Wabunge, tukumbuke wakati fulani TBC ilikuwa inasikika nchi nzima wakati tukitumia teknolojia ya zamani. Bahati mbaya wakati wa mabadiliko haya ya teknolojia mpya, vifaa vingi vile vya zamani sasa havifanyi kazi tena na uwekezaji ulikuwa haujafanyika wa kutosha na ndiyo maana ukweli ni huo kwamba nusu ya nchi yetu inasikika na nusu ya nchi yetu haisikiki. Sasa kwa Shirika la Utangazaji la Taifa kusikika nusu ya nchi, nadhani ni tatizo kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilihakikishie Bunge lako kwamba bajeti ijayo nadhani tutafanikiwa kuleta hapa mpango wa kupata fedha za kutosha wa ku-finance TBC. Uwekezaji mkubwa unahitajika ili kusaidia katika teknolojia, lakini pia kuboresha studio zao na vipindi vyao. Nina hakika Bunge hili likituunga mkono tutakapoleta mapendekezo hayo tutapata pesa za kutosha na tutaliondoa Shirika letu la Utangazaji pale lilipo na ndoto zetu kwamba liwe shirika bora kabisa katika nchi yetu. Inahitajika uwekezaji mkubwa, naamini Bunge litatuunga mkono wakati utakapofika na tutakapoleta hapa wakituunga mkono, tunaamini Watanzania watafurahia huduma nzuri na kazi nzuri ya Shirika la Utangazaji la Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuunga mkono mapendekezo mengi yaliyoletwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge. Nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa. Ahsante sana.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote, waliochangia hoja yangu ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa mwaka 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Mheshimiwa Peter Serukamba ambaye amewasilisha Maoni na Ushauri wa Kamati kuhusu utekelezaji wa bajeti yetu. Pia niishukuru sana Kamati kwa sababu wamechambua mapendekezo yetu na tunawashukuru Kambi ya Upinzani kwa hotuba yao ambayo imewasilishwa na Mheshimiwa Ester Bulaya, tunapokea pia maoni na ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa maoni na ushauri wao na niseme tu kwamba tumepokea hoja nyingi na kwa sababu ya muda sitaweza kupitia book lote hili kumjibu Mbunge mmoja mmoja, lakini katika hatua hii niseme tumepokea maoni na ushauri wenu. Kubwa ambalo limetupa faraja wote Bunge hili tumeungana tunakubaliana kwamba afya ni maendeleo, afya ni elimu, afya ni kilimo, afya ni viwanda, afya ni ulinzi, afya ni uchumi, kwa hiyo, tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja yangu ni 164. Waliochangia kwa kuzungumza ni 61 na kwa maandishi ni 99 na wakati wa mjadala wa Mheshimiwa Waziri Mkuu Waheshimiwa Wabunge wanne pia wamechangia.

Mheshmiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda sitawataja, lakini nitaomba sasa nitoe maeneo makubwa ambayo yameelezwa na Kamati na vile vile yameelezwa na Kambi ya Upinzani pamoja na Waheshimiwa Wabunge. Kabla ya kuondoka katika Bunge hili la bajeti, tutawasilisha majibu ya hoja zote. Nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa ufafanuzi alioutoa katika baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitajikita katika mambo makubwa matano. Jambo la kwanza nitazungumzia rasilimali fedha kwa ajili ya sekta ya afya; pili, nitazungumzia upatikanaji wa dawa; tatu, nitazungumzia afya ya uzazi na motto; na nne nitazungumzia suala la kuthibiti vifo vya watoto wadogo na pia nitazungumzia kuwawezesha wanawake kiuchumi na masuala ya Sheria ya Ndoa ikiwemo sheria zinazolinda haki ya mtoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo limetolewa maoni na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, ni kuhusu rasilimali fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya Sekta ya Afya, kwamba ni ndogo ni chache na haziakisi hali halisi ya changamoto zilizopo katika Sekta ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie hali halisi ya ukusanyaji wa mapato katika nchi yetu. Pili, ningetaka kuwatahadharisha Waheshimiwa Wabunge watofautishe Bajeti ya Wizara ya Afya na Bajeti ya Sekta ya Afya. Kuna mambo mawili niyaweke wazi. Kwa mfumo wa Nchi yetu ambao Mheshimiwa Simbachawene ameuongelea, hela kwa ajili ya kutatua changamoto za sekta ya afya zipo chini ya Fungu 52, lakini pia tutazikuta chini ya Fungu 56 kwa ajili ya Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa pamoja na halmashauri. Kwa hiyo, kuna Mheshimiwa amesema bajeti ya sekta ya afya, ni asilimia tatu, si sahihi. Bajeti iliyotengwa kwa ajili ya Sekta ya Afya ni trilioni 2.2. Nikichukua fedha za TAMISEMI na fedha zilizotengwa chini ya Wizara yangu ni trilioni 2.2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuwapitisha Waheshimiwa Wabunge wakaangalia. Mwaka 2015/2016, Sekta ya Afya ilitengewa shilingi trilioni 1.8; mwaka 2016/2017, Sekta ya Afya imetengewa trilioni 1.9, mwaka 2017/2018 Sekta ya Afya imetengewa shilingi trilioni 2.2. Nafurahi kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba, kati ya vipaumbele vitatu vya Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, sekta ya afya ni ya tatu baada ya miundombinu inafuatia elimu halafu inakuja sekta ya afya. Sisemi kwamba fedha hizi zinatosha, lakini Serikali inajitahidi kwa dhahiri kuonesha kwamba afya za Watanzania ni kipaumbele na ni jambo ambalo tumeliahidi katika Ilani ya Uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija sasa nikiangalia Bajeti ya Wizara ya Afya, Fungu 52, unaiona kabisa dhamira ya dhati ya Serikali ya kuendelea kuwekeza katika afya za Watanzania. 2014/2015, bajeti ya Wizara ya Afya ilikuwa ni bilioni 713; mwaka 2015/2016 bilioni 780; na sasa hivi kwa ajili tu ya Fungu 52 na nimechukua tu, nimeondoa maeneo mengine sasa hivi (2016/2017) inaenda kwenye bilioni 796 na jana nimeomba trilioni 1.1 kwa ajili ya Vote 52. Kwa hiyo, jambo ambalo nataka kuwasisitiza Waheshimiwa Wabunge, ni kweli tumeridhia Azimio la Abuja la kutenga asilimia 15 kwa ajili ya Sekta ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lile ni azimio lazima tuangalie pia vipaumbele vingine vinavyoikabili nchi yetu. Nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge, tutaendelea kushauriana na wenzetu wa Wizara ya Fedha kuhakikisha kwamba wanatoa kipaumbele kwa ajili ya sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo limeongelewa pia na Kamati ya Kudumu ya Bunge pamoja na Kambi Rasmi ya Upinzani pamoja na Waheshimiwa Wabunge Lucy Owenya, Suzan Lyimo na rafiki yangu mpenzi Azza Hilary kwamba tunategemea sana fedha za wafadhili kwa ajili ya kuendesha kutatua changamoto za sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge tumeanza kuwekeza, tumeanza kutumia rasilimali zetu za ndani kwa ajili ya kutatua changamoto za sekta ya afya. Natoa kutoa mfano, mwaka 2014/2015 fedha za ndani kwa ajili ya bajeti ya sekta ya afya zilikuwa bilioni 54; mwaka 2015/2016 bilioni 66; mwaka 2016/ 2017 na hizi ni fedha za maendeleo sizungumzii OC; zimeenda mpaka bilioni 320 na mkiangalia fedha za ndani ambazo sasa tunaomba kwa ajili ya kuetekeleza miradi ya maendeleo ni takribani bilioni 336.

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, ongezeko hili linaonesha ni jinsi gani Serikali inatekeleza ushauri wa Waheshimiwa Wabunge, kwamba ni lazima tutumie rasilimali za ndani kwa ajili ya kutatua changamoto za sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubali katika miradi kwa mfano ya UKIMWI, ukoma, malaria na kifua kikuu asilimia kubwa ya fedha zinatoka kwa wafadhili, lakini kwa mfano dawa za UKIMWI, tumeanza kutenga rasilimali zetu za ndani kwa ajili ya masuala ya UKIMWI. Pia katika masuala ya uzazi wa mpango kwa mara ya kwanza, tumetenga bilioni 14, fedha za ndani kwa ajili ya masuala ya uzazi wa mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihitimishe hoja hii kwa kusema kwamba zipo chngamoto za rasilimali fedha, kwa sababu pia zipo changamoto nyingi za kimaendeleo katika nchi yetu. Nataka kwathibitishia dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais ya kuwekeza katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni faraja kwetu, kwa mara ya kwanza tumekuwa tukipata fedha za kutekeleza miradi, nitatoa mfano wa fedha za dawa. Mwaka 2015/2016 fedha za dawa zilizotolewa ilikuwa ni bilioni 24 tu, nchi nzima iliendeshwa kwa fedha za dawa kwa bilioni 24 tu. Leo ninapoongea jana nilisema ni bilioni 112 lakini tumepata bilioni 20. Kwa hiyo sasa hivi tunaongea bilioni 132 ambazo zimetolewa na Hazina kwa ajili ya fedha za dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala ambalo limeongelewa na Waheshimiwa Wabunge wengi pamoja na Kamati ya Kudumu ya Maendeleo ya Jamii, kuhusu upatikanaji wa dawa. Tunapokea pongezi za Waheshimiwa Wabunge, kwamba tumeboresha upatikanaji wa fedha za dawa, lakini pia tumepokea changamoto kwamba kupatikana kwa fedha za dawa sio kupatikana kwa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ufafanuzi hapa. Katika Hotuba yangu, nimezungumzia upatikanaji wa dawa katika Bohari ya Dawa ni asilimi 81 nimetumia vigezo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi haiwezi kuwa na dawa zaidi ya; tukasema bohari ya dawa ina dawa 3000, 4000 tunaangalia tunaita dawa muhimu zaidi (Essential Medicine) ziko 135. Kwa hiyo, tunaposema upatikanaji wa dawa ni asilimia 81 maana yake katika kila zile dawa 135 asilimia 81 ya dawa hizo zinapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba, hizi takwimu sio za dawa 2,000, dawa 3,000, ni dawa 135 ambazo ndizo za kuokoa maisha. Hata hivyo, sasa tumeenda mbali zaidi, kutokana na maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge, mlitushauri tusiishie tu katika Bohari ya Dawa, ndiyo maana katika bajeti yangu kwa mara ya kwanza tumeenda mpaka katika mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu ambazo nimeziweka katika jedwali la pili, tumeletewa na Waganga Wakuu wa Mikoa na Waganga Wakuu wa Wilaya. Katika hotuba yangu tumeeleza tunaendelea kuboresha mfumo ili tujiridhishe kwamba, takwimu hizi tulizoletewa ni sahihi. Kwa hiyo, nakubali zipo changamoto za dawa kuwepo katika vituo vya afya na katika zahanati. Changamoto ya kwanza, maoteo ya mahitaji yanaletwa kwa kuchelewa. Nitumie fursa hii kuzitaka halmashauri zote kuleta maoteo ya mahitaji ya dawa kama Kanuni ya Sheria ya Manunuzi inavyotaka. Wanatakiwa watuletee by terehe 30 Januari ya mwaka huo kusudi tuweze kuisaidia MSD kununua dawa kwa wakati.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu Mheshimiwa Bobali aliniambia kama haya majedwali yanatofautiana; nadhani hajanielewa. Tutofautishe fedha za dawa na upatikanaji wa dawa. Mheshimiwa Mwenyekiti ni Mwanasheria, moja ya sifa kubwa ya Wanasheria ni kusoma kila kitu na kukitafakari. Kwa hiyo, nimeisoma hotuba zaidi ya mara 10 siletewi. Kati ya jambo ambalo labda Watumishi wa Wizara ya Afya wananichukia ni kwa sababu, nasoma kila kitu, niko tayari hata nirudishe mara 10. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimejifunza kwako wakati nafanya internship yeye alikuwa ndio Mwanasheria Mkuu wa Serikali, lakini pia, nimejifunza kwake wakati ni Mwenyekiti wa Kamati Namba Moja, Kamati ya Kuandika Katiba inayopendekezwa. Kwa hiyo, wanasheria tunasoma, hatuletewi tu ukapitisha. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefurahi sana Mheshimiwa Sannda, shemeji yangu, amezungumzia tatizo la prescription. Kwamba, dawa zipo, lakini saa nyingine wataalam wetu badala ya kuandika dawa zilizopo katika kituo anaamua kuandika dawa pengine zilizo katika duka lake nje ya hospitali, kwa hiyo, hili tutalisimamia. Kwenye kuandika dawa wanatakiwa watu waandikiwe dawa zile ambazo ni dawa muhimu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kuwafahamisha Waheshimiwa Wabunge, dawa zitapatikana kwa sababu tayari tumeingia mikataba mitano na wazalishaji wa dawa. Kwa hiyo, dawa zitatoka moja kwa moja kwa wazalishaji, maana yake zitapatikana kwa urahisi. Nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge na mimi siogopi kuwajibika, nilisema nataka kupimwa kwa mambo ikiwemo upatikanaji wa dawa na hili nataka kuwathibitishia, dawa 135 zitapatikana kwa angalau asilimia 95, hizo nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge, lakini kama kuna mtu atataka dawa ambayo ni brand, si dawa zile 135, hilo siwezi kumthibitishia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliahidi kuboresha upatikanaji wa dawa Ocean Road. Sasa hivi Ocean Road ina dawa kutoka asilimia tatu mpaka asilimia 60. Dawa za Saratani ya mlango wa kizazi ni mpaka asilimia 60. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kulitolea ufafanuzi ni; Mheshimiwa Zedi, tumepokea ushauri wako, lakini taarifa zetu kidogo zinakinzana. Nataka kukuahidi kwamba tutaendelea kufanyia kazi. Nitoe ufafanuzi kwa Waheshimiwa Wabunge, tumeshatoa maelekezo kwa MSD suala la OS (Out of Stock), tumemwelekeza MSD kama umeombwa upeleke dawa ndani ya saa 24 kama hiyo dawa huna, umwambie halmashauri hiyo dawa sina kwa hiyo, nakupa kibali ukanunue kwa mshitiri mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge, halmashauri zetu zianze kuwatambua washitiri (Suppliers) kwamba, kama MSD hana na una hela yako, akupe OS ndani ya 24 hours kusudi mkanunue dawa maeneo mengine. Nawathibitishia dawa zitapatikana na niko tayari kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge hili suala linawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Bulembo, Mheshimiwa Umbulla na Kambi ya Upinzani mmezungumzia kuboresha Bohari ya Dawa. Kama nilivyosema hayo mabadiliko ndiyo tumeanza na kubwa kwa kweli sasa hivi, nashukuru Waheshimiwa Wabunge mmekubali, si fedha ni mifumo. Hii mifumo ndio tunahangaika nayo ikiwemo mifumo ya ugavi na usambazaji wa dawa. Kwa hiyo, Mungu akijalia, nikija kwenye bajeti nyingine tutakuja na takwimu mpaka za zahanati. Tutakuja na takwimu za dawa mpaka katika ngazi ya vituo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa kwa hisia kubwa suala la kuhusu kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi. Walioongea hili ni Kamati ya Kudumu ya Bunge, Kambi Rasmi ya Upinzani, Mheshimiwa Risala, Mheshimiwa Moshi, Mheshimiwa Mgeni, Mheshimiwa dada yangu Amina Makilagi, Mdogo wangu Mheshimiwa Neema Mgaya, Mheshimiwa Ester Mahawe, Mheshimiwa Bukwimba, Mama yetu Mheshimiwa Mama Salma Kikwete na Mheshimiwa Kemilembe. Tunapokea maoni yote kuhusu kuboresha jitihada ili kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe ufafanuzi mmoja; nakubali kwamba vifo vitokanavyo na uzazi bado ni tatizo katika nchi yetu. Naomba niseme, siyo kwamba tumejikwaa wapi? Wala siko hapa kubisha kuhusu takwimu; kwa sababu, ukiangalia sensa limekuwa ni jambo ambalo kidogo limeshtua watu kwa sababu, sensa ya mwaka 2012 ilikuwa inaonesha vifo vya akinamama wajawazito ni 430 katika kila vizazi hai laki moja, lakini takwimu za 2015/2016 ndiyo zinatupa 556.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa Waziri mwenye dhamana, mama, mwanamke, nikisema takwimu hizi sizikubali nitakuwa siwatendei haki Waheshimiwa Wabunge, siwatendei haki wanawake wenzangu wa Tanzania. Nataka kuwathibitishia, ndiyo maana jana nilisema ukiniuliza Waziri wa Afya, Bajeti hii inajibu kero gani? Kama Ilani ya Uchaguzi ya CCM inavyotuelekeza tupunguze vifo; bajeti hii inajibu kupunguza vifo vya akinamama wajawazito. Tumeonesha, kwanza tumewekeza katika huduma za uzazi wa mpango. Kwa sababu wataalam wanasema, uzazi wa mpango unaweza kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi kwa asilimia 30.

Waheshimiwa Wabunge, niwape changamoto, tunapofanya mikutano katika Majimbo yetu, tuhimize masuala ya uzazi wa mpango. Mheshimiwa Shally Raymond umeongea vizuri kwamba, sasa hivi bado kiwango cha uzazi Tanzania ni asilimia 2.7, I mean population growth; na mwanamke wa Tanzania sasa hivi anazaa watoto kati ya watano mpaka sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena nyie watani wangu Wasukuma tena, ndiyo kidogo kule Kanda ya Ziwa matumizi ya uzazi wa mpango hayako vizuri. Nataka kuwaambia, zama… (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaona Wasukuma watani zangu. Nataka kuwaambia kwamba zama zimebadilika. Sasa hivi ukizaa hata watoto wawili, watatu na tumeboresha huduma za chanjo, watoto wale wanaishi. Kwa hiyo, zile zama za kwamba lazima mtu azae watoto 10, 12, lakini tuangalie pia, hao watoto utaweza? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka kukuthibitishia jambo la pili ambalo tutalifanya sambamba na kuimarisha huduma za uzazi wa mpango, tutaimarisha huduma za akinamama wakati wa ujauzito. Ni kweli, unaweza ukaenda katika Kituo cha Afya ukakuta mama mjamzito hapimwi hata wingi wa damu, hapimwi protini, hapimwi hata kama pressure iko juu au haiko juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Simbachawene hayupo, lakini nitoe maelekezo kwa Waganga Wakuu wa Wilaya na Mikoa, hufai kuwa Mganga Mkuu wa Wilaya na Mkoa kama zahanati yako inakosa hata mashine ya kupimia BP kwa mwanamke mjamzito. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu wataalam wanaita albu stick kwa ajili ya kupima mkojo kwa akinamama wajawazito kama protini ni nyingi. Stick 50 zinauzwa sh. 9,000/= tu, DMO unasubiri Mheshimiwa Waziri Simbachawene akuletee sh. 9,000/= kwa ajili ya kununua vipimo vya kupima protini kwa akinamama wajawazito! Kwa hiyo, kati ya eneo ambalo nitakuwa mkali ni suala la huduma za wajawazito wakati wanapohitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili namshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan; yeye amekuwa ndio nguzo yangu, ndio chachu yangu na amekuwa akinipa moyo wa kuendelea kupambana, kwa sababu mimi na yeye na bahati nzuri tulipita wote kuomba kura, eneo ambalo tunataka kukumbukwa na wanawake wa Tanzania ni katika afya ya uzazi na mtoto na hili tutaweza kulifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti hii tumeonesha kwamba tutajenga Benki za Damu tano. Haijawahi kutokea katika bajeti ya Wizara ya Afya. Benki za Damu katika mikoa mitano. Tumeonesha Manyara, tutajenga Katavi, tutajenga Rukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine katika bajeti hii, jana nimeeleza kwa uchungu mkubwa, kwa mara ya kwanza tunatenga fedha zetu za ndani kwa ajili ya huduma za msingi za uzazi za dharura (BIMOC). Kwa hiyo, sasa hivi na ninarudia tena, Waheshimiwa Wabunge nataka muwe mashahidi, hakuna mwanamke mjamzito atafariki kwa kukosa sindano ya oxytocin kwa sababu tu amevuja damu. Hakuna mwanamke mjamzito wa Tanzania atafariki kwa kukosa dawa inaitwa Magnesium Sulphate kwa ajili ya kifafa cha mimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsanteni. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka bajeti hii tunaanza na hizo dawa mbili, lakini mipango yetu baadaye; sababu nyingine ya vifo vitokanavyo na uzazi ni uambukizo. Kwa nini wanawake wajawazito wanakufa? Kwanza wanavuja damu; pili, wanapata kifafa cha mimba; tatu, wanapata maambukizi na nne, wanapata uzazi pingamizi. Kwa hiyo, kwenye kifafa cha mimba na kwenye masuala ya kuvuja damu, tumekuja na hiyo intervention.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uzazi pingamizi, ndiyo maana tumesema tutaboresha Vituo vya Afya 150 ili viweze kufanya upasuaji, huduma za uzazi za dharura, ikiwemo upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni. Mheshimiwa Bobali kwa kweli, unajua kuna jambo ulilisema, Mheshimiwa Waziri, unajua tumekupigia makofi kwa sababu ni mtu wa Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu watu wa Tanga tumeumbwa wanyenyekevu, watu wema, hatujui kujikweza; lakini licha ya kwamba natoka Tanga na unyenyekevu wangu na kutojikweza, lakini haya ninayoyaongea siyo ya kwenye makaratasi, nimetafuta hela kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya kuboresha Vituo vya Afya 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pesa shilingi bilioni 67 ipo tayari kwenye akaunti za Wizara. Tumeshawaelekeza TAMISEMI watuletee mapendekezo ya Vituo vya Afya vya kuboresha. Katika hivyo vituo 100 tutajenga theatre, tutajenga wodi ya wazazi, tutajenga Maabara ya Damu na tutajenga nyumba ya watumishi.

Kwa hiyo, kaka yangu Mheshimiwa Bobali siyo maneno ya kwenye makaratasi, ni maneno ya vitendo na Waheshimiwa Wabunge wanawake nawashukuru sana kwa kuniunga mkono na naamini wote Waheshimiwa Wabunge… (Makofi/Kicheko/Vigelegele)

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, imetosha. Ahsante kwa heshima mliyompa Mheshimiwa Waziri. Tuendelee.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niombe kupitishiwa bajeti, maana naona Waheshimiwa Wabunge wameridhika.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Tano katika kushughulikia tatizo la vifo vitokanavyo na uzazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme suala la vifo vya watoto wenye umri wa chini ya siku 30, Mheshimiwa Kemilembe, Mheshimiwa Mama Salma Kikwete wameliongea sana. Tumetoa maelekezo; tumetoa mchoro mpya kwa ajili ya hospitali. Hatutapitisha mchoro wowote wa hospitali ambao hautakuwa na chumba kwa ajili ya watoto wachanga (neonatal ward). Kwa hiyo, suala la pili, tumeshazielekeza Hospitali za Rufaa za Mikoa zote kuanzisha wodi kwa ajili ya watoto wachanga na sisi Wizara ya Afya tutaendelea kushirikiana na TAMISEMI na Wizara ya Fedha kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya vifaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeongea mambo mengi kwa ajili ya Sekta ya Afya, lakini naomba kabla sijazungumza maendeleo ya jamii, nizungumzie kidogo kuhusu lishe. Lishe ni muhimu sana. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao mmetoa maoni, ushauri, jinsi ya kuboresha huduma za lishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa ambalo tumelifanya kupitia Taasisi ya Chakula na Lishe, tumetengeneza mkoba kuonesha umuhimu wa siku 1,000 za kwanza za mtoto. Maana yake toka mimba ilipotungwa hadi mtoto anapofikia umri wa miaka miwili. Kwa hiyo, tutaendelea kutumia community health workers, wahudumu wa afya wa jamii, tutatumia pia redio na TV ili kuwahamasisha wananchi pamoja na wanawake kuwekeza katika afya zao na watoto wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la chanjo. Taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imesema kuna uhaba wa chanjo. Kuna mambo mengine mnachukua yamepitwa na wakati, mambo ya kwenye mitandao. Hatuna tatizo la uhaba wa chanjo za watoto nchini. Kwa hiyo, hayo yalikuwa ni mambo ya kwenye mitandao yanaletwa katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo chanjo za kutosha na ndiyo maana nimesema, ili kuhakikisha upatikanaji endelevu wa chanjo, tumetenga fedha za chanjo tumezitofautisha na fedha za dawa. Kwa sababu mtu akikosa dawa ataenda kununua kwenye pharmacy, lakini chanjo hazinunuliwi sehemu yoyote, zinatolewa na Serikali tu. Kwa hiyo, tunakiri kuanzia mwaka 2016 kidogo tulikuwa na changamoto, lakini sasa hivi hayo mambo yamepitwa na wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la maendeleo ya jamii. Kubwa ambalo limeongelewa na Waheshimiwa Wabunge, akiwemo Mheshimiwa Faida, kuhusu Benki ya Wanawake Zanzibar, Mheshimiwa Dada yangu Mheshimiwa Faida ameongea kwa uchungu sana, wifi yangu Mheshimiwa Munde, lakini pia Mheshimiwa Neema Mgaya, mdogo wangu amezungumzia suala la Benki ya Wanawake kwa nini haiko Njombe? Kamati ya Kudumu ya Bunge pia, imezungumzia suala la Benki ya Wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea ushauri kwamba, sasa hivi kidogo kuna changamoto katika Benki ya Wanawake, kwa hiyo, tayari tumeshamwomba Mkaguzi Mkuu wa Serikali afanye ukaguzi maalum ili kubaini changamoto zinazokwamisha na kuweka mikakati ya kuboresha. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge mtuvumilie kidogo, kabla hatujaenda kufungua matawi mikoani, tusubiri taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali tuone ni mapendekezo gani atayatoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, suala la riba ya Benki ya Wanawake, naomba nijibu kwamba, tusubiri pia hiyo taarifa ya ukaguzi maalum wa CAG ili tuweze kuboresha utendaji kazi wa Benki ya Wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pia ya Kudumu ya Bunge imezungumzia suala la sheria kandamizi dhidi ya wasichana na watoto, ikiwemo Sheria ya Ndoa. Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria alitueleza changamoto tunazozipata katika kufanyia marekebisho Sheria ya Ndoa. Ninachoweza kuwaahidi Waheshimiwa Wabunge ambao mmeongea kwa hisia kubwa, wakiwemo Mheshimiwa Sebastian Kapufi, Mheshimiwa Juliana Shonza, Mheshimiwa Taska Mbogo, Mheshimiwa Ester Mahawe, Mheshimiwa Aida Khenani, Mheshimiwa Suzan Lyimo, Mheshimiwa Richard Mbogo na Mheshimiwa dada yangu Sophia Mwakagenda, ni kwamba, nitaendelea kushirikiana na wenzangu Serikalini kuangalia ni jinsi gani tunaweza kufanyia marekebisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri nami ni Muislamu, ziko changamoto zinazohusiana na masuala ya dini. Nimekutana na Mashehe na wameniambia ukisoma vizuri Kitabu cha Mwenyezi Mungu unaweza ukasema wala hakuna tatizo katika kufanyia marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe changamoto ambayo nimeshampelekea Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali; Bangladesh asilimia takribani zaidi ya 90 ya Bangladesh ni Waislamu, lakini wamepitisha Sheria ya Ndoa mwezi Januri mwaka huu, 2017 ambapo wao sasa wamefanya hivi, wameongeza umri wa ndoa, wamesema umri wa ndoa kwa mwanamke utakuwa miaka 18 na kuendelea, lakini wakasema under special circumstances ndoa chini ya umri wa miaka 18 inaruhusiwa.

Kwa hiyo, nitaenda kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali angalau kutoa pendekezo hili, angalau na-raise minimum age of marriage kutoka 14 years to 18 years, lakini unatoa exceptions kidogo. Kwa hiyo, nimeangalia Malawi wenzetu wamepitisha Sheria ya Ndoa…

MHE. JOHN J. MNYIKA: (Hakusikika)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Hapana Mheshimiwa Mnyika. Kuna watoto saa nyingine, Bangladesh wamesema kama ni mtoto under 18 years na under a special circumstances such as pregnancy, wameandika kama amepata mimba. Kwa hiyo, hiyo kidogo naweza nikawashawishi wenzangu ndani ya Baraza la Mawaziri na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwamba tunaweza tukabadilisha. Kwa sababu kilio kikubwa ni minimum age of marriage (umri wa kuolewa). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum, Njombe, amezungumzia sana kwamba tumesema watoto ni asilimia 51, kwa hiyo, mnafanya jitihada gani za kuwekeza kwa watoto wadogo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rose Tweve nataka kukuthibitishia, kati ya jambo kubwa katika kulinda haki za watoto wanaonyonya; na Mheshimiwa Jenista nakushukuru sana; tulipeleka kwa Mheshimiwa Jenista mapendekezo ya kufanyia marekebisho ya Kanuni za Sheria za Kazi na Ajira; kwa sababu ile sheria ukiiangalia inasema mwanamke akimaliza maternity leave anaruhusiwa kunyonyesha, lakini sheria haisemi ananyonyesha kwa muda gani.

Mheshimiwa Jenista nakushukuru sana, tumepeleka mapendekezo, sheria inasema hivi, kwamba mwanamke mjamzito anaruhusiwa kunyonyesha baada ya maternity leave kwa muda wa miezi sita ndani ya masaa mawili na muda wowote ndani ya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili tutaendelea kuwataka waajiri kuzingatia mabadiliko ya sheria ambayo Serikali ya Awamu ya Tano imeyapitisha kuhakikisha watoto wananyonyeshwa na mama zao. Kwa hiyo, sasa hivi ni miezi sita baada ya martenity leave na masaa mawili, muda mwanamke mwenyewe mfanyakazi atakaosema. Akisema anaingia kazini saa 4.00 badala ya saa 2.00 sheria inamruhusu, akisema atatoka masaa mawili kabla ya muda wa kazi kwisha, sheria inamruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisipozungumzia suala la ukatili dhidi ya watoto, sitawatendea haki watoto wa Tanzania. Nataka kuwathibitishia, licha ya kwamba tumetunga sheria kali dhidi ya vitendo vya ukatili dhidi ya watoto, lakini bado vinajitokeza kama nilivyoonesha katika taarifa yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kubwa ni kuendelea kuhamasisha jamii, walezi na wazazi. Mheshimiwa Mbunge aliongea jambo zuri sana, sasa hivi hata kama ni mila zetu mgeni kulala na mtoto mdogo; nataka niwaambie siyo salama kwa mgeni; awe ni mjomba, awe ni baba mdogo, kulala na mtoto wa kiume. Kwa sababu, kwa mujibu wa taarifa zetu, ubakaji dhidi ya watoto na ulawiti unafanywa na watu wa karibu ndani ya familia zetu. Kwa hiyo, tuchukue tahadhari ya kuwalinda watoto wetu dhidi ya vitendo vya ukatili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo ni mengi kama nilivyosema, lakini tunawashukuru sana kwa michango yenu. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuchangia na kwa ushirikiano mzuri mnaotupatia, lakini kipekee nirudie kuwashukuru sana wafadhili wetu ambao wanatuwezesha kutekeleza miradi yetu ya Sekta ya Afya, ikiwemo wanaochangia Mfuko wa Pamoja wa Afya, niliwataja jana; Denmark, CDC, Ireland, Canada pamoja na Korea ya Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee jana sikuweza kuwashukuru Shirika la Afya Duniani ambao kwa kweli wanatupa msaada mkubwa katika kutekeleza masuala ya afya, hasa masuala ya kitaalam. Vile vile tunawashukuru sana UNICEF kwa michango yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, sitaki kupigiwa kengele, niseme kwamba tumepokea changamoto. Nimalize moja, la Sheria ya Wazee, ni kweli, tuliahidi Sheria ya Wazee tutaileta Bungeni. Tumekwama kwa sababu, zipo taratibu ndani ya Serikali za kutengeneza sheria. Kwa hiyo, litakapomalizika tutakuja katika Bunge lenu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema jana, sote ni wazee watarajiwa. Ni jukumu la kila mtu ikiwemo Serikali kuhakikisha tunaweka mazingira mazuri na salama kwa ajili ya kuwalinda na kuwatunza wazee wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sasa, naomba kutoa hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kuniamini kusimamia sekta hii ya afya na maendeleo ya jamii, nimhakikishie Mheshimiwa Rais nitashirikiana na Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndungulile, Naibu Waziri ili kuhakikisha Watanzania wanakuwa na afya njema na hivyo kuweza kushiriki katika kujiletea maendeleo yao na maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayofanya katika eneo hili la uchumi na fedha lakini hasa kwa kuleta mapendekezo ya mpango wa maendeleo ya Taifa kwa mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri walioutoa hasa katika kuboresha upatikanaji wa huduma za afya nchini, ikiwemo kujenga jamii ya Watanzania inayojali na kuheshimu haki, ustawi na maendeleo ya wanawake, wazee na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge lakini nitajikita sana kwa Dada yangu Mheshimiwa Susan Kiwanga. Niliposikiliza mchango wake nikasema hivi huyu amesoma huu mpango au amesoma hajauelewa? Kwa sababu anasema kwamba mipango yetu haizingatii mahitaji halisi ya Watanzania. Unasema hivi huyu anazungumzia Watanzania gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua Mheshimiwa Dkt. Mpango ataeleza uhusiano mkubwa sana kati ya ujenzi wa uchumi wa viwanda na maendeleo ya watu, ikiwemo kuboresha afya, ikiwemo elimu, ikiwemo vijana na kila kitu. Lakini nataka ni-summarize kwa kitu kimoja, maendeleo ya watu, maendeleo ya jamii, msingi wake mkubwa ni maendeleo ya kiuchumi. Dkt. Mpango na timu yako songeni mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua Tanzania ya viwanda ndani ya huu mpango ni halisi. Maana nimesoma hotuba yao wanasema Tanzania ya viwanda uhalisia au ndoto? Ni uhalisia! Tunasonga mbele wame-panic ndiyo maana sasa wanatafuta sababu zisizo na maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ndiyo maana nasema amesoma? Ukiangalia ukurasa wa 51, Mheshimiwa Mpango na timu yake wanasema kufunganisha maendeleo ya viwanda na maendeleo ya watu, sasa niache nimuoneshe kwenye sekta ya afya, wananchi wa Mlimba wanataka nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mlimba hawataki bora huduma, wanataka huduma bora za afya. Mheshimiwa Mpango katika kitabu hiki anasema kwamba kuboresha upatikanaji wa dawa, vifaa na vifaa tiba. Huu ndiyo Mpango! Sasa namshangaa Mheshimiwa Susan Kiwanga, kabla ya Serikali ya Awamu ya Tano haijaingia madarakani Ifakara walikuwa na fedha za dawa shilingi milioni 19 tu, mwaka jana tumewapa shilingi milioni 120 za dawa, mwaka huu tunawapa shilingi milioni 164, halafu anasema Mpango huu haujazingatia mahitaji ya wananchi. Najiuliza, Dkt. Mpango mimi naunga mkono hoja kwa sababu najua hata huko Mlimba, Ifakara tutaongeza fedha zaidi ya hizi ambazo umeweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili unajiuliza anasema siyo vipaumbele vya Watanzania. Unajiuliza, Watanzania wanataka nini? Watanzania wanataka wote tutibiwe Muhimbili siyo nje ya nchi. Mheshimiwa Dkt. Mpango anatuonesha hapa kwamba ataboresha huduma za matibabu ya kibingwa. Ndiyo maana nimesema ni kuchanganyikiwa, wanaona tunasonga mbele. Nitoe mfano, Watanzania tutatibiwa Muhimbili, nataka kutoa mfano Hospitali ya Taifa ya Muhimbili pale ICU tumeongeza vitanda vya wagonjwa mahututi kutoka 21 mwaka 2015 hadi vitanda
75. Tumeongeza vyumba vya upasuaji Muhimbili kutoka vyumba 13 hadi vyumba 20. Watu walikuwa wanasubiri miaka miwili kufanyiwa upasuaji. Sasa hivi watu wanasubiri miezi minne na tunategemea kushusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upasuaji wa watoto, Muhimbili walikuwa wanafanya upasuaji wa watoto 15 kwa wiki, sasa hivi wanawafanyia watoto 50 kwa wiki. Mheshimiwa Dkt. Mpango anasema haya ni mapendekezo, nataka kuboresha huduma za matibabu ya kibingwa. Sasa unasema mpango huu haujazingatia mahitaji halisi ya wanananchi. Unajiuliza hivi huyu kweli anazungumza anachokijua kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kutoa mfano mwingine. Watanzania wanataka nini kama nilivyosema?

Watanzania wanataka wote wapate huduma za matibabu ya kibingwa. Tumeanza, kuna wazazi wana watoto wana matatizo ya kutosikia, Muhimbili leo wamepandikiza vifaa vya kusikia cochlear implants, Mtanzania gani wa kawaida ataweza kutumia shilingi milioni 80 mpaka shilingi milioni 100 kwenda China? Lakini Muhimbili watapata Watanzania wote!

Mheshimiwa Mwenyekiti, habari njema, wasiwe wanasema tu, habari njema ni kwamba kabla ya tarehe 30 Desemba, tunaanza upandikizaji wa figo. Watanzania wanataka kuona huduma za matibabu ya kibingwa wote wanapata na siyo wenye fedha, huduma hizi zitapatikana nchini, Dkt. Mpango hongera sana nakuunga mkono kwa mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nani alikuwa anafahamu upasuaji lazima watu wapelekwe India? Jakaya Kikwete Cardiac Institute ilikuwa inapasua mgonjwa mmoja kwa siku, leo wagonjwa watatu kwa siku. Watanzania wote wanapata huduma hizi. Haya mambo ni kuanzia mwaka 2016 mpaka leo ndani ya miaka miwili mambo makubwa sana yamefanyika katika kuboresha sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa nasema hivi huyu anasoma nini? Watanzania wengi wanapata matatizo ya saratani. Zamani unaenda pale Ocean Road, wana vitanda 40 tu kwa ajili ya huduma ya saratani ya maji (chemotherapy) leo kuna vitanda 100, wagonjwa 100 wanatibiwa kwa wakati mmoja. Mheshimiwa Dkt. Mpango nashukuru kwamba tunaenda kununua kifaa kinaitwa PET scan kwa ajili ya tiba ya uchunguzi na uchunguzi wa matibabu ya saratani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nashangaa hivi huyu, lakini ninamshukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Bobali ametoa mchango mzuri, jamani wagonjwa wengi wa saratani wanaongezeka. Mna mpango gani wa kuongeza elimu? Huu ndiyo mchango ambao ninauona una lengo la kujenga. Siyo mchango wa kusema hakuna vipaumbele. Kaka yangu Bobali nakushukuru sana. Nataka kukuhakikishia tutaendelea kutoa elimu juu ya wananchi kujikinga na saratani na tulichokifanya sasa hivi, tumeongeza pia vituo vya kuwezesha hasa wanawake kwa sababu saratani kubwa inayoongoza ni saratani ya mlango wa kizazi kwa asilimia 34 na saratani ya matiti asilimia 12. Kwa hiyo, Serikali ya Awamu ya Tano imeongeza vituo vya kuwezesha wananchi kupima kutoka 343 hadi 443, haya ndiyo wanayotaka Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie jambo la mwisho, anazungumzia afya ya mama na mtoto wananchi wanakufa, tunajua. Lakini hivi ukijenga tu majengo ndiyo watu watapona? Sisi tumejikita kwenye kuboresha kwanza huduma. Tumesema kama kweli hiki ni kituo cha afya tunakitaka kiwe kituo cha afya na ndiyo maana kupitia Awamu ya Tano, wakati Mheshimiwa Dkt. Magufuli hajaingia madarakani, vituo vya afya 500 vya Serikali ni 109 tu vinavyotoa huduma za uzazi za dharura ikiwemo upasuaji. Mwaka wa pili wa Magufuli tunaongeza vituo 170 na Waheshimiwa Wabunge mmepata barua. Hii ndiyo tunataka, lakini kwa nini wanawake wanakufa? Kwa sababu pia wanavuja damu, wana upungufu wa damu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Mpango anatuambia anataka kuongeza upatikanaji wa dawa na chanjo. Sasa hivi chanjo, dawa za uzazi salama (Oxytoxin) kwa ajili ya kuzuia mwanamke kuvuja damu magnesium sulphate kwa ajili ya kuzuia kifafa cha mimba na phehol kwa ajili ya kuongeza damu zinatolewa bure! Hii ndiyo wananchi wa Mlimba wanataka. Najua Mheshimiwa Jafo ataongelea ujenzi wa zahanati na vituo vya afya, lakini sisi tumejikita hizo huduma zilizokuwepo ziwe ni huduma bora siyo bora huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema siyo vipaumbele vya wananchi. Labda Dada yangu Mheshimiwa Susan Kiwanga wewe na familia mna hela, lakini Watanzania nikikutwa HIV positive nianze dawa mara moja. Tumeanza Sera ya Test and Treat. Mtanzania yeyote atakayepima na
kukutwa na maambukizi ya virusi vya UKIMWI anapata dawa siku hiyo hiyo tunamwanzishia, halafu anasema Mpango huu haujazingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namaliza la mwisho, Mheshimiwa Susan Kiwanga; TB kabla Mheshimiwa Magufuli hajaingia madarakani kulikuwa na kituo kimoja tu cha kutoa matibabu ya TB sugu, Kibong’oto Hospital. Leo tuna vituo 18 ikiwemo Ifakara, ikiwemo Ifakara kituo cha Kibaoni. Halafu mtu anauliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha Dkt. Mpango nakuunga mkono kaka yangu, Naibu Waziri na wataalam wote wa sekta ya fedha. Endeleeni, mkisikia watu wanasema sema wame-panic kwa sababu wanajua Tanzania ya viwanda inafikiwa. Kwangu tukifikia Tanzania ya viwanda najua maendeleo ya sekta ya afya yanafikiwa na Watanzania watakuwa na afya bora na ustawi na hivyo kushiriki katika kujiletea maendeleo yao na maendeleo ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii kwa ushauri wao mzuri kuhusu utendaji kazi wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua hii niseme kwamba tumepokea ushauri na maoni ya Kamati yote yaliyotolewa na niahidi mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba tutayazingatia kwa sababu lengo la ushauri ambao umetolewa ni kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, namba mbili, tumepokea pongezi za Kamati kuhusu kazi nzuri inayofanywa na taasisi zetu kama walivyoona; TFDA, MSD, MOI, MNH na JKCI na kupitia hatua hii niahidi Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwamba Serikali ya Awamu ya Tano itaendelea kuchukua jitihada hasa za kuimarisha upatikanaji wa huduma za matibabu ya kibingwa, matibabu bobezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano katika Taasisi yetu ya Moyo ya Jakaya Kikwete wameendelea kufanya kazi nzuri ya kupunguza rufaa za wagonjwa nje ya nchi kutoka rufaa za wagonjwa 89 mwaka 2016 hadi wagonjwa wawili tu kwa mwaka 2017. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana ya kazi hii nzuri ambayo wanafanya taasisi zetu sio kwamba tu Serikali itapunguza gharama na kuokoa fedha, lakini maana yake Watanzania wote maskini au tajiri ana accessibility ya kupata huduma za matibabu bobezi, kwa hiyo ni suala la usawa kwa watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge pia kwa kutambua kazi ya Muhimbili, bahati mbaya kwamba ile CT Scan ni siku mbili lakini inafanya kazi nzuri na tutambue kwamba Muhimbili wanafanya mabadiliko makubwa ya kutoa huduma za kibingwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimwambie Mheshimiwa Mtolea tu kwamba tunafunga CT Scan kwenye Taasisi yetu ya Mifupa ya MOI kwa hiyo itakuwa ni backup, pale CT Scan ya Muhimbili itakapoharibika, basi ya MOI itafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sasa nijikite katika maoni yaliyotolewa na Kamati, kama nilivyosema ni mengi, lakini nizungumze mambo makubwa matano. Jambo la kwanza, ni kuhusu hali ya upatikanaji wa dawa. Tunashukuru Kamati kwa kuona jitihada ambazo zimefanyika ndani ya Serikali na tunakubali kwamba bado zipo changamoto chache katika upatikanaji wa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme, changamoto kubwa ya upatikanaji wa dawa ilikuwa inachangiwa na upatikanaji wa fedha, hakukuwa na fedha za dawa. Sasa hivi fedha za dawa zipo katika halmashauri zetu, zipo katika zahanati zetu, zipo katika vituo vya afya na zipo katika hospitali zetu za rufaa za mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Lubeleje changamoto ambayo tunayo, ukiangalia stock level ya MSD na lingine ambalo nilitolee ufafanuzi, hatuwezi kuangalia upatikanaji wa dawa zote, tunaangalia zile dawa muhimu (essential medicine) ambazo ziko 135, na kwa mujibu wa taarifa ya MSD dawa hizi zinapatikana zaidi ya asilimia 80.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyokuwepo ni suala la mfumo wa ugavi na usambazaji wa dawa. Nitoe mfano, katika maoteo ambayo tumeyapokea kutoka kwenye halmashauri inaonekana kwamba tunahitaji nchi nzima paracetamol kopo 7,000 lakini kiuhalisia tunauza paracetamol kopo moja yenye vidonge 1,000 kopo 16,000, kwa hiyo, huu ni mfumo ule ambao wa maoteo kutoka halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dawa ya amoxicillin, kwa mujibu wa maoteo ambayo tumeyapata kutoka halmashauri, inaonekana kwamba tunahitaji kopo 6,500 lakini kiuhalisia tunauza kopo 19,000. Kwa hiyo, niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge na Kamati tutaendelea kuzihimiza halmashauri kuleta maoteo halisi ya dawa ambazo zinahitajika katika halmashauri zao na kuleta maoteo hayo kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo tutalifanya, tumepata ufadhili, tumenunua magari zaidi ya 180 ambayo yatatumika kusambaza dawa katika sehemu mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kubwa, tumezindua mfumo Standard Treatment Guideline, mwongozo wa matibabu na orodha ya dawa muhimu. Kwa sababu saa nyingine hali ya upatikanaji wa dawa unachangiwa pia na prescription, daktari anaandika dawa ambayo haipo kwenye mwongozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la kaka yangu anayesema kuna dawa za China, dawa za India, dawa za UK, Tanzania tunatumia generic medicine, tunatumia dawa ambazo ni generic na zimepitishwa na WHO. Kwa hiyo, saa nyingine mgonjwa anaenda pale anataka dawa ambayo anaitaka yeye haipo katika mwongozo. Kwa hiyo, tutaendelea kutoa mafunzo kwa watoa huduma za afya, hasa Waganga na Madaktari, kuhusu kuzingatia mwongozo wa matumizi ya dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la NHIF, niseme kwamba tumepokea pia ushauri wa Kamati kwamba tuharakishe mchakato wa kuleta Bungeni sheria itakayomlazimisha kila Mtanzania kuwa na bima ya afya. Nakubaliana na Kamati kwamba ni kweli ni Watanzania wachache ambao wako katika bima ya afya, NHIF kuna Watanzania milioni 3.3 sawa na asilimia saba, CHF ni asilimia
11.7 na bima za afya binafsi ni asilimia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika Watanzania 100 ni Watanzania 32 tu ndio wanapata huduma za matibabu bila kutoa fedha cash, maana yake wanapata changamoto katika kupata huduma, lakini pia mtu anayetumia papo kwa papo analipa zaidi kuliko mtu mwenye kadi ya bima ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niithibitishie Kamati ya Bunge kwamba, Serikali tayari tumeshapata uzoefu wa nchi mbalimbali, WHO wametusaidia, World Bank wametusaidia, tunajua kipi kimefanya kazi Rwanda kipi hakijafanya kazi Ghana, lakini tunakubali kwamba tutaenda kutembelea, lakini kabla ya kwenda kutembelea nchi hizo tunapanga kuitisha semina ya wadau ili waone Ghana wamefanya vipi, Rwanda wamefanya vipi, Philippines wamefanya vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli ya Serikali ni kwamba bima ya afya ndiyo mwelekeo, ndiyo mhimili wa kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la afya ya uzazi na mtoto ni suala la kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Nne na niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge suala la kutoa elimu ya uzazi hasa kwa wasichana tumelipa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana tulikuwa na kikao mimi na Waziri wa Elimu na Waziri wa TAMISEMI, tumeamua kwamba tutaangalia mitaala kuhusu masuala ya afya ya uzazi ili watoto wetu waweze kujua maumbo yao na waweze kujikinga na magonjwa. Vile vile tumeongelea suala la kuwa na Walimu walezi katika shule zetu na tayari pia mwongozo wa kuwafundisha Walimu unaangaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa ambalo pia tunalifanya katika huduma ya afya ya uzazi ni kwamba Wizara itaendelea kuimarisha upatikanaji wa huduma za uzazi za dharura na nithibitishie Serikali ni moja, Wizara ya afya tutatafuta fedha lakini fedha hizi sisi tutazipeleka TAMISEMI na ndiyo maana tumepata fedha kwa ajili ya kuboresha vituo vya afya 100 katika Halmashauri mbalimbali. Tumepata fedha kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya vituo 100, Ubalozi wa Denimark wametupa fedha kwa ajili ya vituo vya afya 39 na basket fund tumepata fedha kwa ajili ya vituo 19. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme Wizara ya Afya haitajenga vituo vya Afya au Zahanati, kazi hiyo ni ya TAMISEMI sisi tunaingia katika suala la kuimarisha ubora wa huduma na hasa katika kuimarisha huduma ya afya ya mama na mtoto. Kwa hiyo, hela sisi tutazipeleka TAMISEMI lakini tunafanya vizuri na Mheshimiwa Jaffo, vituo vyote vya afya wanakaa wataalam wetu kwa pamoja na wanasema fedha hizi tuzipeleke wapi na hizi tuzipeleke wapi. (Makofi)

MheshimiwaMwenyekiti, suala la fedha za WDF ni kwamba Hazina tumeshafanya majadaliano lakini niwaimize Waheshimiwa kwamba suala la kuwawezesha wanawake kiuchumi ziko kwa kiasi kikubwa ni ile asilimia tano ya Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la vitambulisho kwa wazee, niseme kwamba tumefanya kazi na tumewatambua wazee takribani milioni 1,600,000 na wazee takribani laki 462 tumeshawapa vitambulisho. Ufafanuzi vitambulisho hivi havitolewi na Wizara ya Afya. Vinatolewa na Halmashauri na kuna Halmashauri zinafanya vizuri; Kigamboni, Msalala, Ubungo, Ikwiriri nitumie fursa hii kuwataka Wakurugenzi wote kuhakikisha wanawapa wazee vitambulisho vya matibabu bure. Pia niweke wazi hii ni hatua ya mpito lengo letu ni wazee wote kupata Bima za Afya pale ambapo tutaanza Bima ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea malalamiko kuna baadhi ya Halmashauri zina waambia wazee wachangie hela ya picha Sh.1,000. Tukimgundua Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo anawachaji wazee kwa ajili ya kitambulisho cha matibabu bure tutapeleka jina lake kwa Mheshimiwa Rais iliaweze kuchukua hatua. Hatutakubali wazee wetu kudhalilishwa kunyanyaswa na sisi sote ni wazee watarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho ni human resource for health watumishi katika Sekta ya Afya tunakubali kwamba changamoto ipo lakini tayari Serikali imeanza hatua tumeajiri mwaka huu watumishi takribani 3,152 na tumewasambaza katika vituo mbalimbali. Naamini kwamba na Waziri wa Utumishi ananisikia lengo letu ni kuhakikisha kwamba hakuna kituo au zahanati ambayo itaongozwa na mhudumu wa afya au mtu ambaye hana sifa. Tunataka Kama zahanati lazima awe ni Clinical of Assistant au Clinical Officer.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hili suala la watumishi dada yangu Benardetha Mushashu kuhusu hospitali za rufaa za mikoa na dada yangu Nuru Bafadhili kuhusu hospitali ya rufaa ya Bombo Mheshimiwa Rais ametukabidhi kuziendesha hospitali za rufaa za Mikoa tumesha-identify, tumeshachambua, tunafundisha Madaktari Bingwa katika fani saba za kipaumbele na Daktari Bingwa wa akinamama na magonjwa ya wanawake ya uzazi, Daktari Bingwa wa watoto, Daktari Bingwa wa upasuaji, Daktari Bingwa wa usingizi na Wanadiolojia wa mionzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeshapata fedha kutoka Global Fund na tunaanza mwaka huu kusomesha zaidi ya madaktari 150, tunawachukua ndani ya Serikali kwa sababu ina kuwa rahisi baada ya kumaliza kurudi kufanya kazi katika mazingira haya, lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa mzungumzaji)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mwisho niseme kwenye watumishi tunategemea kuwa na Community Health Workers hawa wataweza pia kuimarisha masuala ya lishe na masuala ya uzazi wa mpango. Kwa hiyo, tunategemea kuwa nao wawili kila kijiji na tayari Mheshimiwa Mkuchika anakaribia kumaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana Waheshimiwa Wabunge tunawashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kusimama hapa, nianze kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja yangu ya kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya fedha kwa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa mwaka 2018/2019. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya kipekee nimshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Maendeleo na Huduma ya Jamii, Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba ambaye amewasilisha Maoni na Ushauri wa Kamati kuhusu utekekelezaji wa kazi za Wizara kwa mwaka 2017/2018 pamoja na bajeti ambayo tunaipendekeza Bunge lako Tukufu kuipitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawashukuru Kamati kwa kututia moyo, kwa kupongeza Wizara yangu na kwa niaba ya wafanyakazi wote wa sekta ya afya katika ngazi zote nchini Tanzania na maendeeo ya jamii kwa niaba yao napenda kupokea pongezi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kutoa majibu ya hoja mbalimbali ambazo zimewasilishwa na Waheshimiwa Wabunge niwatambue Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwa kuzungumza na kwa maandishi; na kwa sababu kanuni zinanibana kuwataja niseme tu kwamba hoja yangu imechangiwa na Wabunge 117, kati ya hao Wabunge 73 wamechangia kwa kuzungumza na Wabunge 44 wamechangia kwa maandishi. Aidha, Waheshimiwa Wabunge nane wamechangia kuhusu sekta ya afya wakati wa mjadala wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kutoa ufafanuzi, niseme kwamba tumepokea maoni, ushauri na mapendekeo ya Kamati na Waheshimiwa Wabunge kuhusu kuboresha huduma za afya. Vilevile tumepokea pongezi zenu na mimi ninasema pongezi hizo zirudi kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ambaye kwa dhamira yake ya dhati ameamua kuwekeza kwenye afya ya Watanzania; na hii ni kutokana na kuamini kwamba hatuwezi kujenga Tanzania ya viwanda bila kuwa na Watanzania wenye afya bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ambaye ametoa kipaumbele katika sekta ya afya. Kabla hajaingia madarakani tunaona kwamba bajeti ya sekta ya afya imeongezeka. Wakati hajaingia madarakani ilikuwa shilingi trilioni 1.8, mwaka wa kwanza wa Mheshimiwa Magufuli imepanda mpaka shilingi trilioni 1.9 na mwaka wa pili wa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli bajeti ya Sekta ya Afya imepanda mpaka shilingi trilioni 2.2.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini kwamba Wizara ya Fedha wanaendelea kufanya tathmini na uchambuzi wa bajeti ya mwaka 2018/2019. Sina shaka hata kidogo kwamba sekta ya afya itaendelea kuwa kipaumbele kati ya vipaumbele vitatu vya Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunavyofahamu changamoto za sekta ya afya katika nchi yetu ni nyingi, hasa katika mazingira ambayo tuna idadi kubwa ya wanawake ambao wanazaa watoto wengi. Kiwango cha uzazi ni asilimia 5.1. Vilevile tuna mzigo wa magonjwa, zamani tulikuwa na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kama kipindupindu, TB, HIV lakini sasa hivi tunabeba mzigo wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza ikiwemo kisukari, magonjwa ya moyo na saratani.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na changamoto hizi, sekta ya afya katika kipindi cha miaka miwili na nusu ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli imepata mafanikio makubwa sana. Tumeona leo katika historia ya nchi yetu Tanzania tumeanza kupandikiza figo katika Hospitali yetu ya Muhimbili na hospitali yetu ya Benjamin Mkapa. Lakini tumeona watoto wanaozaliwa na matatizo ya kusikia wakiweza kupandikiziwa vifaa vya kuongeza usikivu katika Hospitali yetu ya Muhimbili wakati zamani miaka miwili na nusu iliyopita huduma hizi zilikuwa hazipatikani katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kaka yangu James Mbatia aliongelea kuhusu Medical Tourism in Tanzania. Nataka kusimama mbele ya Bunge lako tukufu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge ndani ya Magufuli Medical Tourism Tanzania itawezekana na itawezekana kwa kipindi kifupi tu. Tunamaliza kufunga mitambo ya LINAC katika Hospitali yetu ya Ocean Road ambayo ni mionzi ya kisasa kwa ajili ya tiba ya saratani. Tunakaribia kununua kifaa cha Pet Scan, hakipo Kenya, hakipo Uganda, hakipo Zambia, hakipo Malawi. Kwa hiyo, watu wa kutoka nchi za Afrika watakuja Tanzania kwa sababu ya uwekezaji mkubwa ambao anaufanya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo ya Mheshimiwa Rais ni mengi, lakini nimalize tu kwa kusema tumeona uwekezaji mkubwa katika afya ya mtoto, asilimia 97 ya watoto wote Tanzania wanapata chanjo, na sisi tumejidhatiti tutamfikia kila mtoto popote alipo ili kuhakikisha anapata chanjo ili kuweza kumkinga na magonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo sasa nijibu hoja za Waheshimiwa Wabunge na nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa ufafanuzi ambao ameutoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na hoja kubwa za Kamati. Kamati imezungumzia kuhusu makubaliano ya Abuja ambayo yalifanyika mwa 2001 ambapo nchi za Afrika zilikubaliana kutenga asilimia 15 ya bajeti zao za nchi katika ajili ya kutatua changamoto za sekta ya afya. Suala la Abuja Declaration ni dhamira si kwamba ni kitu kina-bind, kinabana nchi wanachama, ni dhamira ya nchi za Afrika kuwekeza kwenye sekta ya afya. Hata hivyo kama nilivyosema tumeona uwekezaji ambao Serikali ya Awamu ya Tano imekuwa ukifanya katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, tumefanya utafiti, ni nchi moja tu ya Afrika ambayo bajeti yake ni asilimia 15 ya bajeti ya nchi. Kwa sababu kama nilivyosema changamoto za nchi za Afrika ni nyingi, kuna masuala ya maji, barabara, kilimo,na maji. Kwa hiyo muhimu kile kidogo ambacho tunakipata muhimu kwetu sisi sekta ya afya ni kuhakikisha kwamba kinatumika kikamilifu bila kupotea katika mambo ambayo hayana tija kwa Watanzania hasa Watanzania wanyonge. Kwa hiyo, nashukuru maoni ya Kamati kwamba haijafika lakini ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba tunafikia asilimia 15 ya bajeti nzima ya Serikali katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati imeongea suala la kwamba bajeti ya Wizaya ya Afya kwa mwaka 2018/2019 imepungua ukilinganisha na ya mwaka 2018/2019.

Waheshimiwa Wabunge, mwaka jana wakati nawasilisha bajeti hapa mlini-challenge kwamba Mheshimiwa Waziri bajeti yako kwa kiasi fulani inategemea wafadhli wa nje, je, wafadhili wa nje wakijitoa mtatatua vipi changamoto za sekta ya afya?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kilichotokea bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka huu kwa fedha za ndani imeongezeka kutoka bilioni 628 mwaka jana hadi bilioni 681. Punguzo tunaloliona ni fedha za nje na hii ni kuonesha dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ya kutaka kupunguza utegemezi kwa wadau wa maendeleo katika kutatua changamoto za watanzania ambao wao ndio wamempa ridhaa ya kumchagua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ukiangalia domestic allocation zimepanda, lakini kwenye forex zimeshuka, na ni kwa sababu tunataka kuanza kujipima wenyewe leo donor akijitoa tutaweza kutatua changamoto zetu kwa kiasi gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo limeongelewa na Kamati ni suala la kwamba inashauri Serikali kutoa fedha zote zilizotengwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018 kama ambavyo Bunge lako tukufu liliidhinisha. Serikali hii ni sikivu na kwa sababu bado hatujamaliza mwaka wa fedha wa 2017/2018 tunaamini kwamba tutaweza kupata fedha kutoka Wizara ya fedha na mipango kwa ajili ya kutekeleza miradi ambayo tumejiwekea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala ambalo Kamati ya Bunge imelizungumzia, suala la lishe, kwamba lishe sio suala la wizara ya afya pekee bali ni suala mtambuka na Serikali ichukue hatua za makusudi za kupunguza janga la lishe. Tunapokea ushauri na maoni ya Kamati kuhusu suala hili, na mimi nikiwa Waziri mwenye dhamana nimefarijika sana kuona Kamati ya Bunge na Wabunge wote wanatoa kipaumbele katika suala la lishe. Kwa kweli suala la lishe na mimi nakubaliana nanyi si suala la mchezo kwa sababu kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2015/2016 kiwango cha udumavu kwa watoto wetu ni asilimia 34. Of course tumepiga hatua ukiangalia kutoka mwaka 2010 ilikuwa ni asilimia 42.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini maana ya watoto kuwa na udumavu ni nini, tunawekeza katika ujenzi wa Tanzania ya viwanda, tunakosa watoto ambao wanaweza wakawa na ubunifu, udadisi lakini ambao wanaweza wakawa na afya bora kwa ajili ya kutatua changamoto za kujenga Tanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama Serikali tumechukua mikakati na hatua mbalimbali chini ya uratibu wa Mheshimiwa Waziri Mkuu na yeye mwenyewe alisimamia kikao cha kwanza cha wadau wa masuala ya lishe kutoka wizara zote ambapo sasa tunatekeleza mpango jumuishi wa kitaifa wa utekelezaji wa masuala ya lishe kwa kipindi cha 2016/2017 mpaka 2020/2021. Mpango huu umeweka vipaumbele mbalimbali ambavyo Mikoa pamoja na Halmashauri zitatekeleza katika kuinua hali ya kiwango cha lishe nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nimshukuru sana Waziri wa Fedha Dkt. Mpango, hayupo hapa, lakini baada ya kuona tatizo la lishe aliahidi na ameyatekeleza. Katika Wizara ya Fedha sasa hivi kuna Afisa mahususi ambaye anahusika na masuala ya lishe, yeye kazi yake ni kuangalia bajeti zote hizi ni kiasi gani masuala ya lishe yamepewa kipaumbele. Pia tumepeleka maafisa lishe sasa hivi wako katika mikoa, wako katika halamashauri pia wako katika ngazi mbalimbali za wizara mtambuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumezindua pia mpango wa kuhamasisha mabadilko ya tabia miongoni mwa jamii ijulikanayo kama Mkoba wa siku 1000 za mwanzo, kwa sababu kwa mujibu wa wataalam wa afya siku 1000 za mwanzo za mtoto ndizo siku muhimu katika maisha yake. Pia tumeongeza idadi ya viwanda vinavyoongeza virutubishi, tunasema food fortification kutoka viwanda 13 hadi viwanda 21. Sasa hivi viwanda ambavyo vinazalisha ngano, mafuta ya kula, unga wa mahindi na chumvi lazima viwe na virutubisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ambayo tunaipata na mimi nikiri, kwa sababu wanakoboa unga katika lower level kwenye vijiji na mitaa, kwa hiyo, kidogo kuwabana kwamba ule unga ambao wanazalisha uwe na virutubisho inakuwa ngumu. Lakini kubwa ambalo tumeliona ni kutoa elimu ya lishe katika jamii kwa sababu hata ukiangalia mikoa ambayo ina viwango vikubwa vya udumavu unakuta ni mikoa ambayo ina uzalishaji mkubwa wa chakula. Kwa mfano, tukiangalia Rukwa wana udumavu asilimia 56 wakati ndio wazalishaji wakubwa wa chakula. Tukiangalia Njombe, Ruvuma, Iringa, Katavi na Mbeya. Kwa hiyo, sisi tumeona ni suala la elimu kwa jamii hasa kwa siku zile ambazo mama anajiandaa kubeba ujauzito.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa ambalo tutaendelea nalo pia ni kuhimiza uzalishaji na matumizi ya mazao lishe katika mahindi, viazi vitamu, maharage na mihogo; lakini ambalo sasa nataka kulifanya baada ya kuwasikiliza Waheshimiwa Wabunge ni kufanya tafiti ya kitaalam ili kubaini sababu au chanzo cha hali ya lishe nchini. Kwa sababu nimesema Rukwa, Katavi, Iringa, Njombe wanazalisha chakula kwa nini tuna udumavu. Kwa hiyo nataka kupata majibu ya kisayansi kuhusu hali ya viwango vya utapiamlo katika baadhi ya mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala kubwa ambalo limeongelewa na Wabunge wote, Wabunge wanawake na wanaume ni suala la huduma za mama na mtoto. Tunawashukuru sana Kamati kwa kupongeza jitihada ambazo Serikali inafanya katika kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma za afya ya mama na mtoto ikiwemo huduma za upasuaji wa dharura.

Waheshimiwa Wabunge wameniuliza Mheshimiwa Waziri kwamba vifo vitokanavyo na uzazi vinaongezeka tumetoka kwenye 432 mwaka 2015/2016 vimefika mpaka vifo 556.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunatoa majibu haya Disemba, 2016 tulitaka kubishana, tulibishana kidogo tukasema tumekosea wapi, pamoja na jitihada zote ambazo Serikali imefanya kwa nini vifo vya akina mama wajawazito vimeongezeka? Baada ya kutafakari tukaamua hakuna maana ya kubishana, awe amekufa mwanamke mmoja bado kwetu sisi ana umuhimu mkubwa sana. Kwa hiyo, tukajikita katika kuchukua hatua za kuboresha huduma ya mama na mtoto na ndiyo maana sasa hivi tukaandika andiko na tukapata fedha kwa ajili ya kuboresha vituo vya afya ili viweze kutoa huduma za uzazi za dharura ikiwemo upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Watanzania wanataka kumuhukumu Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli mumuhukumu kwa jitihada ambazo amezifanya katika kuboresha huduma za upasuaji za dharura. Mwaka jana ni asilimia 21 tu ya vituo vya afya vya Serikali vinavyoweza kufanya upasuaji, lakini tutakapofika Disemba tutakuwa na asilimia 53 ya vituo vya afya vya Serikali vitakavyoweza kufanya upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ambayo iko mbele yangu sasa kama sekta ni kuhakikisha tunakuwa na wataalam, watumishi wenye ujuzi ambao wataweza kuwahudumia akina mama wajawazito ambao watapata matatizo ya uzazi wa dharura. Tumeshaanza kuwafundisha wauguzi katika masuala ya utaalamu wa usingizi ambao tutawasambaza katika vituo hivi ambavyo vinajengwa theatre. Tumesambaza ambulance 50 katika mikoa mbalimbali pamoja na kuimarisha huduma za damu salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hatua inayokuja sasa hivi kama nilivyosema ni kuimarisha huduma za uzazi wa mpango. Kwa sababu wataalam wamenifundisha Wizara ya Afya kwamba endapo tutakuwa na idadi kubwa ya wanawake wanaotumia uzazi wa mpango tutaweza kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi kwa asilimia 30.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge tuhimize matumizi ya uzazi wa mpango kwa wanawake kwa sababu sasa hivi ni asilimia 32 tu ya wanawake nchini Tanzania ambao wanatumia huduma za kisasa za uzazi wa mpango. Pia tutaendelea na jitihada za kuimarisha huduma wakati wa ujauzito na hapa tunahitaji lengo letu wanawake wajawazito angalau wahudhurie kliniki mara nne kama wataalam wanavyoshauri. Sasa hivi wanawake wanahudhuria kliniki mara nne ni asilimia 51.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo eneo ambalo tutaliboresha pia pale ambapo mama mjamzito anaenda kliniki tunataka apate huduma bora badala tu ya kupoteza muda wake. Tunawaambia wenzetu mama mjamzito anatoka kilometa 20, 30 hata 40 anafika kwenye kituo hapimwi wingi wa damu, hapimwi maambukizi aliyokuwa nayo, hapewi huduma mtoto amekaa vizuri, kwa hiyo, tunatoka kwenye miundombinu tunaenda kwenye ubora wa huduma. Tunataka kuona huduma bora kwa akina mama wajawazito. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa mama na mimi nimeingia labour mara mbili, nataka kuwaahidi Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tutahakikisha huduma kwa mama mjamzito zinaendelea kuboreka.

Mheshimiwa Naibu Spika, limejitokeza suala la delivery pack kwamba zinauzwa, na pia tutoe ufafanuzi kwamba matibabu kwa wajawazito je, ni bure au si bure?

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Afya na mimi nimeuwa nikilisisitiza hivi si hili kwamba matibabu kwa wajawazito, huduma kwa wajawazito ni bure kuanzia wakati anapohudhuria kliniki mara tu baada ya kujigundua ni mjamzito, lakini pia wakati wa uzazi na wiki sita baada ya kujifungua. Kwa hiyo suala la kwamba akina mama wajawazito wanatozwa fedha za kumwona daktari nalikemea mara moja, na niwatake watoa huduma za afya zote Waganga Wakuu wa Mikoa kusimamia agizo hili, kusimamia sera hii. Ni marufuku kum-charge mama mjamzito fedha pale ambapo amekwenda katika kituo cha kutoa huduma za afya kwa ajili ya kupata fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la delivery pack, Waheshimiwa Wabunge mama mjamzito hatoi fedha ya kumwona daktari, hatoi fedha ya dawa, hatoi fedha anapojifungua wala hatoi fedha ya kufanyiwa upasuaji. Kwa hiyo delivery packs zitaendelea kuwepo kaatika vituo vya kutoa huduma za afya kwa kuzingati rasilimali fedha ambayo Serikali au kituo kinacho. Nimeongea hapa, kwa mwaka tunakuwa na wajawazito milioni mbili delivery pack 21,000. Waheshimiwa Wabunge, naomba mnisaidie shilingi bilioni 40 ambazo kila mwaka tutazitenga kwa ajili ya kutoa delivery pack. Sisi tulichokifanya pale ambapo kuna fedha za Serikali na mama mjamzito ataenda atakuta vifaa hivi atapewa bure. Sasa suala la delivery pack ni suala la mama mjamzito kujiandaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, uzazi si dharura ni miezi tisa, uzazi ni miezi tisa, kwa hiyo, ni sawa sawa na mama anavyojiandaa kununua nguo ya mtoto, kununua kanga, akiikuta delivery park kwenye kituo atasema Alhamdulillah, asipoikuta inakuwa ni sehemu ya maandalizi. Hata hivyo nataka kuendelea kuwaahidi, tunaelekea kwenye Bima ya Afya kwa kila mtu (Universal Health Coverage). Kundi ambalo tutaanza nalo pale ambalo tutatoa Bima ya Afya, kwa sababu tumesema akina mama wajawazito huduma ni bure tutawapatia huko mbeleni, kwa hiyo, ndio kundi ambalo tutalipa kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ina maana tunaweza tukaangalia utaratibu wa kupata kadi za bima ya afya ili waweze kupata huduma bila vikwazo vya fedha. Tumeanza kwa kushirikiana na Serikali ya Ujerumani, huduma hii tunaiita Tumaini la Mama, inafanyika katika mikoa ya Lindi, Mtwara, Tanga na Mbeya. Msije mkasema Tanga nimeikuta hata kabla sijawa Waziri, kwa hiyo, ni eneo ambalo tumeanza nalo, lakini tunaamini kwamba tutaweza kuboresha huduma hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine lililohusu masuala ya afya ya mama na mtoto ni suala la chanjo ya kuwakinga wasichana na saratani ya mlango wa kizazi. Nafurahi kuona kwamba Waheshimiwa Wabunge mmelipokea vizuri na wengi mmetusisitiza kwamba tukatoe elimu kwa jamii na sisi tutaenda kutoa elimu kwa jamii.

Tunaomba Wabunge, hasa Wabunge wenzangu wanawake, kumuuguza mgonjwa mmoja wa saratani ya mlango wa kizazi tunatumia shilingi milioni tano, hatujahesabu gharama familia ambayo inaingia katika kumuuguza mgonjwa yule. Nadhani tutakuja kufanya semina muone, endapo tutawachanja wasichana na chanjo hii ya saratani ya mlango wa kizazi ndani ya miaka 10 saratani ya mlango wa kizazi itakuwa historia katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe rai tena kwa wazazi na walezi wenzangu, tuwapeleke binti zetu kupata chanjo hii. Mimi mwenyewe binti yangu ana miaka 13. Tumeanza na miaka 14 kwa sababu chanjo hizi mahitaji ni makubwa sana. Waziri wa Afya wa Nigeria kwa mwaka anahitaji dozi milioni 20, mimi nikiwachanja mabinti wote wa miaka tisa mpaka 14 nahitaji dozi kama milioni 3.9. Kwa hiyo, mzalishaji amesema nitaweza kuwapa dozi za wasichana 600,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tumeona badala ya kusubiri mpaka mwakani na Mheshimiwa Kiteto Koshuma umeongea vizuri, watoto wetu wanaanza utundu mapema. Tunaweza tukasema tusubiri mwakani tuwachanje wote miaka tisa mpaka 14 hawa 14 kuna asilimia fulani tutawapoteza. Kwa hiyo, tumesema tuanze na miaka hii 14 halafu sasa mwakani tutawatoa wasichana wote na Mheshimiwa Angellah Kairuki ameniahidi na yeye watoto wake amewachanja tena amewachanja dozi tatu.

Kwa hiyo, akina mama Wabunge nitaomba tutoke mbele, tuwashawishi wanawake wenzetu kwamba chanjo hii ni salama. Chanjo hii itapigwa dozi mara moja kwenye sindano halafu baada ya miezi sita itarudia. Sambamba na hayo tutaongeza jitihada pia za kuwapima na kutoa huduma za matibabu ya awali kwa wanawake wajawazito.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati pia iliongelea suala la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na ambao wameshauri kwamba tuufanyie marekebisho pamoja na kuja na vifurushi vya bima. Ushauri huu tunaupokea na mimi mwenyewe nimekuwa nikiwa-challenge Bima ya Afya, kwamba kwa nini msifanye kama kampuni za simu, jipimie, unajipimia. kwamba unataka huduma za afya mpaka Muhimbili, unataka huduma za afya mpaka Hospitali ya Bombo Tanga au unataka huduma za afya mpaka ufike KCMC.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimefurahi kwamba ndani ya siku chache tutazindua vifurushi mbalimbali ili wananchi wajipimie katika kupata huduma za matibabu. Pia tumeona kuna bima ya afya, total afya kadi 50,400 kwa mtoto matibabu mwaka mzima mpaka Muhimbili, mpaka MOI mpaka JKCI. Kwa hiyo, tumekubaliana badala ya kusubiri mzazi alipe shilingi 50,400 kwa mara moja nimewaelekeza NHIF waweke utaratibu, mzazi leo ana shilingi 5000 anachangia, ana shilingi 10,000 anachangia, baada ya miezi fulani tumeweka utaratibu wa miezi mitatu kadi itakuwa imekamilika mnampa bima ya afya mtoto anakuwa na uhakika wa matibabu kwa mwaka mzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilikuwa Nzega kwa Mheshimiwa Bashe, tukawauliza boda boda kuna bima ya afya ya kikundi tunaita kikoa, kwa nini hamkati? Wakaniambia Waziri shilingi 78,600 hatuwezi, lakini ukiniambia nitoe shilingi 2,000 kila siku nitaweza kuchangia shilingi 2,000. Kwa hiyo tumeona kwamba inawezekana kuongeza idadi ya Watanzania watakaokuwa na bima ya afya lakini lazima pia na sisi tuwe wabunifu. Kwa hiyo, tunaupokea ushauri wako Mheshimiwa Peter Serukamba pamoja na Wabunge wote ambao mmeutoa katika kuongeza idadi ya Watanzania ambao wana Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumejiongeza, tunafanya mazungumzo na vyama vya ushirika, Wabunge wa Mikoa ya Kusini mmezungumzia suala la korosho. Kwa hiyo, tayari tunasema wakati mkulima anauza korosho basi pale pale aweze pia kukatwa na Bima ya Afya.

Kwa hiyo tumechukua hili zao la korosho, pamba pamoja na kahawa, na vyama vya ushirika vimeshakubali, kwamba pale ambapo wananchi wanapewa fedha zao watakatwa pia ili kupata Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge matibabu ni gharama na matibabu ni gharama narudia tena tukisema kila mzigo ubebe Serikali hatuwezi kufika, tutakuwa tunajidanganya. Kama wapiga kura wetu wanaweza kununua vocha ya simu shilingi 500 kila siku siamini kwamba wanashindwa kuchangia shilingi 500 hiyo hiyo ili waweze kupata Bima ya Afya.

Kwa hiyo, tutaendelea pia kuhamasisha ili wananchi waone kwamba kuwa na Bima ya Afya unakuwa na ukahika wa kupata matibabu kabla ya kuugua. Mtu maskini akiumwa leo atauza baskeli yake, atauza shamba, atauza vitu alivyokuwa navyo, lakini mwenye Bima ya Afya ataweza kupata huduma za matibabu bila kikwazo cha fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya Kamati pia ilikuwa ni mapambano dhidi ya UKIMWI, kwamba upatikanaji wa fedha za Serikali kwa ajili ya ununuzi wa dawa za kufubaza UKIMWI tunategemea wenzetu kutoka nje. Tumepokea changamoto hii na nitumie fursa hii kuwatoa hofu Waheshimiwa Wabunge kwamba chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Jenista tumeanzisha extra fund ambayo itaweza sasa kugharamia huduma mbalimbali zinazolenga UKIMWI.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Jenista nakushukuru sana uliweza kunipa cheque ya milioni 260 ili tuweze kununua dawa kwa ajili ya magonjwa nyemelezi kwa wenye matatizo ya UKIMWI. Kwa hiyo, suala hili ninamini kabisa kwamba ndani ya muda mchache; na sasa hivi pia, kama nilivyosema tunakamilisha mkakati wa kugharamia huduma za afya (financing for health sector). Kwa hiyo katika mkakati huu pia tumebainisha maeneo ambayo tunaweza tukapata vyanzo mbalimbali kwa ajili ya kugharamia huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilikuwa naongea na Waziri mwenzangu wa South Africa, wao katika kila asilimia fulani ya fedha ambayo ni kwa ajili ya sukari inaenda kwa ajili ya kugharamia pia changamoto za sekta ya afya. Juzi tulikuwa pia na watu wa Ghana na wenyewe wametupa nao uzoefu wao kwamba asilimia mbili ya VAT pia inaenda kugharamia huduma za afya. Kwa hiyo, tutaendelea kufanya mashauriano na wenzetu Hazina ili kuona ni kiasi gani basi; Mheshimiwa Bashe amezungumza wale watu maskini ambao kwa mujibu wa takwimu za World Bank ni asilimia kama 28 ya Watanzania ndio maskini sana. Kwa hiyo, tutaangalia ni kiasi gani sasa tutaweza kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kugharamia changamoto za afya ikiwemo masuala ya UKIMWI na HIV. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala ambalo pia limeongelewa na Waheshimiwa Wabunge hasa Mheshimiwa Lubeleje ni suala la afya ya mazingira. Nimpongeze sana Mheshimiwa Lubeleje kwamba hawa Mabwana Afya wamewekwa katika maeneo ambayo si sahihi. Mheshimiwa Lubeleje nimepokea hoja yako na ndiyo maana ukiangalia hotuba yangu ya bajeti ya mwaka jana na mwaka huu. Mwaka huu baada ya chanjo eneo la pili ambalo nimeliweka ni suala la afya na usafi wa mazingira. Kwa sababu tunapoteza fedha nyingi sana katika kutibu magonjwa ya kuhara kipindupindu na minyoo na magonjwa mengine ilhali tungeweza kuyaepuka pale ambapo Watanzania watazingatia kanuni za usafi wa mazingira pamoja na usafi wa afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni kweli kaka yangu Shangazi tutaendelea pia na kampeni yetu ya usichukulie poa nyumba ni choo na lengo la kampeni hii ni kutaka kubadilisha mtazamo na mwamko wa Watanzania kuhusu usafi wa mazingira ikiwemo vyoo bora. Watanzania wana nyumba nzuri, utamwona ana tv screen inchi sijui hamsini na ngapi, nenda kaangalie choo chake, nenda kaangalie vyoo katika stand zetu, nenda kaangalie vyoo katika vituo vyetu vya kutoa huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwangu mimi baada ya suala la chanjo kwa watoto suala la afya na usafi wa mazingira ndicho kipaumbele cha pili. Kwa hiyo, natuma salamu kwa Mabwana Afya wote katika Halmashauri na mikoa, haitakuwa business as usual maana Mabwana Afya wetu muda mwingi wanapoteza kwenda kukagua butcheries na mahoteli kwa sababu wanapata fedha. Kwa hiyo tumeambizana tutakaa chini na tutatoa miongozo, tunataka waende kwenye kaya na kuhamasisha masuala ya afya na usafi wa mazingira badala ya kujikita kwenda kukagua butcheries na hoteli kwa sababu pia kuna ka- asilimia fulani wanaweza kupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa Lubeleje pia tumeangalia suala la kada ile ya kama ulivyosema environment health officers na assistant, kwa hiyo tutalijadili Wizarani, na tumeamua kwamba baada ya kulijadili tutakuja na mapendekezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala ambalo pia linahusu kuhusu afya ya mazingira na hili nimpongeze sana mdogo wangu Mheshimiwa Maria Kangoye amezungumzia suala la hedhi salama. Tunakubaliana, ndiyo kipaumbele pia kama kweli tunataka kuimarisha usafi na afya ya mazingira. Kwa hiyo, suala hili la hedhi salama hasa kwa wasichana na wanawake wa vijijini tunalipa kipaumbele. Sisi kubwa ambalo tutalifanya ni kuongea na wenzetu wa Wizara ya Fedha kama ulivyosema kuweza kuwaomba tutoe kodi katika taulo za wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini hili litawezekana, kwa sababu tusidanganyane tutatoa taulo za kike kwa sasa hivi kwa watoto wangapi, kila mwaka tunaongeza Watanzania wapya milioni mbili, na ninyi mnafahamu asilimia 51 ya wananchi ni wanawake. Kwa hiyo hili suala tunalichukua, lakini tutaendelea kuimarisha tu mazingira kwenye shule zetu pamoja na vituo vya kutoa huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, limeongelewa pia suala la ongezeko la magonjwa yasiyo ya kuambukiza ambalo Waheshimiwa wameongea, Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete pia dada yangu Mheshimiwa Dkt. Jasmine Tisekwa. Pamoja na utoaji elimu ya afya kwa jamii pamoja na kupima magonjwa tutaendelea, na ndiyo maana tunaimarisha pia kitengo chetu cha elimu ya afya kwa umma. Mheshimiwa Rita Kabati alizungumzia mpango wa kutoa chanjo ya HPV kwa watoto wa kiume pia kwa watoto ambao wana umri zaidi ya miaka 15.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeipokea hoja hii, lakini kwetu sisi tumeangalia kundi au rika ambalo ndilo liko kwenye hatari. Kwa hiyo, nchi zenye uwezo zinatoa chanjo hii kwa wavulana, zinatoa chanjo hii kwa wasichana wa zaidi ya miaka 15, sisi tunajikuna pale ambapo tunaweza. Kwa hiyo, tumeona tuanze na umri huu wa miaka tisa hadi miaka 18.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maendeleo ya jamii, kuna hoja imetolewa kuhusu mimba za utotoni ikiwemo mikakati gania ambayo tunafanya, tunaendelea kutoa elimu kwa wasichana, wazazi na walezi kutoa elimu ya sexual and reproductive health education (elimu ya uzazi na afya ya uzazi kwa wasichana) na nimeongea na Mheshimiwa Profesa Ndalichako tunaangalia pia, curriculum (mitaala yetu) ili sasa katika shule zetu tuwe na walimu, lakini pia tuwe na somo ambalo hawatafanya mitihani, lakini watoto watajua A, B, C, my right my protection, angalao wajue my body my pritection. Kwa hiyo, ni eneo ambalo tunaona linaweza kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa Mwenyekiti Najma, amezungumza kuwahasi watu ambao wanabaka na kulawiti watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimelitafakari suala hili, nikaangalia Sheria ya Makosa ya Kujamiiana ambayo imeingizwa katika Sheria ya Kanuni za Adhabu, tumeweka adhabu kali miaka 30, kuanzia miaka 30 mpaka kifungo cha maisha kwa mtu ambaye atakutwa amebaka. Mimi naona adhabu hii ni kali kwa kiasi fulani. Kwa hiyo, sisi tujikite katika kuelimisha jamii ikiwemo wasichana na wazazi kutimiza wajibu wao kwa malezi, lakini na watoto wa kike pia kujitambua na kujilinda na kuwajengea uwezo watoto kutoa taarifa pale ambapo wanafanyiwa vietndo vya ukatili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dalaly Kafumu amezungumzia masuala ya vituo vya afya na Wabunge wengi, kwamba, kuboresha vituo vya afya. Mheshimiwa Naibu Waziri amelijibu suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba, ujenzi wa miundombinu ya afya, zahanati, vituo vya afya na hospitali za wilaya upo chini ya Serikali za Mitaa, TAMISEMI. Sisi kazi yetu ni kusimamia sera kuhakikisha kwamba kuna miundombinu ya kutoa huduma za afya. Hata hivyo pale ambapo tunaona kuna changamoto. Kama nilivyosema tumekuja na hoja ya uzazi salama, kwa hiyo, sisi tukaamua tutafute fedha za kuboresha vituo vya afya, ili viweze kutoa huduma za uzazi za dharura. Kwa hiyo, ni eneo ambalo..., kwa mfano, tunataka kuja na mpango wa kuboresha huduma ili tuweze kuwahudumia wagonjwa wa kifua kikuu, wagonjwa wa UKIMWI, lakini pia na ugonjwa wa malaria.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mama Mheshimiwa Riziki Lulida sijakusahau, balozi wa malaria katika Bunge hili. Malaria ni changamoto na ninafurahi kuwataarifu Waheshimiwa Wabunge tarehe 25 Aprili tunaenda Kasulu na moja ya shughuli ambayo tutaifanya ni kuzindua hali ya malaria nchini Tanzania. Habari njema ni kwamba kiwango cha malaria kimepungua na tutatoa takwimu. Tutaendelea pia kujikita katika afua za kuzuwia badala ya kusubiri kutibu. Ni kweli tunatumia fedha nyingi sana kwa ajili ya kuwatibu watu malaria wakati tungeweza kutumia viuadudu vile ambavyo vinazalishwa Kibaha kwa ajili ya kuuwa mazalia ya mbu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge kwa hiyo nimemua katika fedha za dawa ambazo tunazipeleka kwenye Halmashauri tutakata baadhi ya fedha kwa ajili ya kununua viuadudu vya kuuwa mazalia ya mbu. Kwa sababu badala ya kusubiri wanunue wenyewe hawanunui, kwa hiyo, tutawakata kwenye fedha za dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kuhusu mapambano ya VVU na UKIMWI, Mheshimiwa Mama Salma Kikwete kwamba suala la dawa za kufubaza VVU hazipatikani kwa wakati, Mheshimiwa Mama Salma tutafuatilia, lakini kati ya eneo ambalo kwa kweli tuna uhakika wa kupata dawa ni suala pia la dawa za ARV na tunawashukuru sana wadau wetu ambao wanatupa fedha katika kutoa ARV ambao ni Global Fund pamoja na PEFA wa Marekani.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala pia la ongezeko la UKIMWI Dodoma, Mheshimiwa Fatma Toufiq. Ni kweli, hata mimi Tanga maambukizi kwa mujibu wa takwimu za THIMS yameongezeka kutoka 2.4 percent mpaka asilimia tano. Kwa hiyo pia tutafanya tathmini kwenye hii mikoa ikiwemo Tanga na Dodoma, ni kwa nini maambukizi ya VVU na UKIMWI yameongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, sitaki kupigiwa kengele, lakini kwa kweli, niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa maoni na ushauri, na tutajibu hoja zenu kwa maandishi. Kipekee nirudie tena kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri Dkt. Faustine Ndugulile, kwa sababu wote mnafahamu hata kabla hajawa Naibu Waziri alikuwa ni mmoja wa washauri wangu katika kutatua sekta ya afya. Kwa hiyo, ninamshukuru sana kwa ushirikiano mzuri ambao ananipatia, vile vile nawashukuru sana wataalam wote, madaktari, wauguzi wote wanaotoa huduma katika vituo vyenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuwa mkali sana ninapoona hatutoi consideration, tunafanya vitendo vya kuwaumiza watoa huduma za afya. Sisemi kwamba, wote ni wazuri, wapo wabaya, lakini ni wachache…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, wale wazuri lazima tuwape heshima yao, lazima tuwathamini. Kwa mfano wauguzi, kazi ya wauguzi wanne inafanywa na muuguzi mmoja na yeye ni binadamu anachoka. Kwa hiyo, nitaomba sana viongozi wenzangu wa Serikali tuwaheshimu na kuwathamini madaktari na wauguzi kwa sababu wanatoa huduma za afya na wanatibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Rais, Katibu Mkuu Mpoki na Mama Sihaba Nkinga na Mganga Mkuu wa Serikali na wote Profesa Janabi anatuletea heshima kubwa sana katika nchi yetu na Mwenyezi Mungu ninaamini Medical Tourism itaanza Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nianze kuwashukuru Wajumbe na Wenyeviti wa Kamati kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameifanya ikiwemo kuleta mapendekezo mazuri katika kuboresha utendaji wa sekta ya afya na maendeleo ya jamiii. Kipekee niipongeze sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii pamoja na Kamati ya Masuala ya UKIMWI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme katika hatua hii tumepokea maoni na ushauri wa Kamati. Nataka kukiri mimi na Mheshimiwa Naibu Waziri tumekuwa tukipata ushirikiano mzuri sana, maoni mazuri sana kutoka kwa Kamati na ndiyo maana sekta ya afya inafanya vizuri sana nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, nitoe ufafanuzi katika maeneo makubwa manne. Eneo la kwanza ni kuhusu sekta ya maendeleo ya jamii, Kamati imeshauri kwamba katika kuimarisha uratibu wa mashirika yasiyo ya kiserikali tuanzishe kanzi data ya NGOs. Tumeanzisha na tumeanza zoezi hili mwezi wa Juni, 2018 na tunataraji kwamba tutazindua katika Bunge lijalo la Aprili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kuanzisha Kitengo cha Udhibiti Ubora wa NGO, tayari tunacho Kitengo cha Uratibu na Ufuatiliaji wa NGO lakini nataka kukiri tunahitaji kuongeza nguvu ili sasa kazi ya kufuatilia hela za NGO, kazi gani wamefanya na wanafanya tuweze kuzifahamu vizuri. Mwezi wa Oktoba, 2018 tumepitisha kanuni mpya kwa ajili ya kutaka uwazi na uwajibikaji wa mashirika ya NGO juu ya hela ambazo wanazipata. Kama tunavyofahamu NGO nyingi zinaomba fedha kwa kutumia majina ya Watanzania maskini. Kwa hiyo, tumepitisha kanuni tunataka watoe taarifa kila baada ya miezi sita hela hizo zimepatikana kiasi gani na zinatumika wapi na katika masuala mangapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwa upande wa sekta ya afya, tumepokea ushauri kuhusu kukamilisha mchakato wa kuanzisha Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote. Mimi na Naibu Waziri tumefarijika sana kwamba suala hili linaungwa mkono na Wabunge wote. Nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba tupo katika hatua za mwisho za kukamilisha Muswada, tunategemea utatupa nafasi Bunge la Bajeti, najua hatujadili sheria lakini tulete sheria hii muhimu kwa sababu Serikali ya Magufuli imefanya kazi kubwa katika kuboresha upatikanaji wa dawa, kujenga hospitali, kuboresha vituo vya afya pamoja na vifaa tiba. Kwa hiyo, ni kweli wananchi hawatapata huduma bora za afya kama hawana uwezo wa kifedha. Bima ya Afya itakuwa ndiyo suluhisho la kuhakikisha kwamba wananchi wote wanapata huduma za afya bila kikwazo cha fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la vifurushi tunalikamilisha, tumeanza na vifurushi mbalimbali, tunataka wananchi wajipimie wenyewe huduma za afya ambazo wanataka kuzipata. Kama unataka ufike mpaka Muhimbili utajipimia kufika Muhimbili na kama unataka ufike Dodoma Regional General Hospital utafika. Kwa hiyo, tunakamilisha na tumeanza kwa mfano kifurushi kwa ajili ya wakulima (Ushirika Afya) kwa ajili ya wakulima wa korosho na kwa Sh. 76,800 mkulima wa korosho anapata uhakika wa matibabu mwaka mzima. Tumeanza pia bima ya afya kwa ajili ya watoto (Toto Afya Card) kwa Sh.50,400. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ester Mmasi suala la Bima ya Afya ya Wanafunzi ni Sh.50,400 tu. Kwa hiyo, vyuo binafsi wanafanya wizi kama wanachukua Sh.100,000 ya Bima ya Afya ya Wanafunzi. Tutaweka utaratibu wanafunzi walipe moja kwa moja NHIF badala ya kulipa kupitia vyuo kwa sababu bima ni Sh.50,400. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo tumelipokea ni kwamba tufanye tathmini ya ustahamilivu ya Mfuko wa Bima ya Afya. Tumefanya tathmini kwa takwimu za mwaka 2016, nataka niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge tunaweza kutoa huduma za afya hadi mwaka 2029. Ila pale ambapo tutaongeza idadi kubwa ya wananchi kujiunga na bima ya afya, naamini mfuko utakuwa una ustahamilivu mzuri na hivyo kutoa huduma mbalimbali za afya.

Mheshimiwa Spika, suala la UKIMWI, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri Ikupa amejibu baadhi ya hoja lakini nataka kukazia hoja moja ya Mheshimiwa Jacqueline Msongozi. Ile hoja ni muhimu sana kwa sababu tafiti zinaonyesha kwamba huduma za tohara kwa wanaume inakinga maambukizi ya VVU kwa hadi asilimia 60. Kwa hiyo, tusidharau wanaume kufanya tohara kwa wale ambao hawajafanyiwa tohara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa mikoa ya kipaumbele ya Iringa, Njombe, Tabora, Mbeya, Songwe, Rukwa, Katavi, Ruvuma, Shinyanga, Simiyu, Mwanza, Geita, Kagera, Singida, Kigoma, Mara na Morogoro huduma za tohara kinga ni bure.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, nakuongezea dakika mbili itaje mikoa taratibu, umeenda haraka hatujaisikia hii mikoa. (Makofi/Kicheko)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, huduma za tohara ni bure katika Mikoa ya kipaumbele ambayo ni 17 na Mikoa hii inajumuisha Iringa, Njombe, Tabora, Mbeya, Songwe, Rukwa, Katavi, Ruvuma, Shinyanga, Simiyu, Mwanza, Geita, Kagera, Singida, Kigoma, Mara na Morogoro; Dodoma haipo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilitaka tu kusisitiza kwamba ni tafiti za kitaalam zimeonyesha kwamba tohara kwa wanaume inaweza kuzuia maambukizi ya VVU hadi kwa asilimia 60. Kwa hiyo, tulitilie maanani suala hili.

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Msongozi ameongelea suala la kuambukiza saratani ya mlango wa kizazi. Saratani ya mlango wa kizazi inaambukizwa kutoka kwenye kirusi cha mwanaume kinaitwa Human Papilloma. Kwa hiyo, pale ambapo mtu ana mkono wa sweta inamuweka pia katika hali ya kuweza kuchochea mazingira ya kirusi kile cha Human Papilloma ambacho ndiyo kinasababisha saratani ya mlango wa kizazi. Kwa hiyo, nitoe rai kwa wanaume ambao hawajapata tohara waone suala hili kwamba ni la kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tumeenda mbali, tumeanzisha Mpango wa Tohara kwa Watoto Wachanga kati ya siku 1 hadi siku 60. Lengo letu sasa ni kuhakikisha kwamba suala la tohara kinga linakuwa endelevu na tumeanza kutekeleza katika mikoa sita ya Njombe, Iringa, Tabora, Mbeya, Songwe na Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la tiba, Kamati imetushauri kutoa ruzuku kwa hospitali ikiwemo Jakaya Kikwete, MOI, MNH na Hospitali za Rufaa za Mikoa. Niseme sisi kama Serikali kwa mfano mwaka jana katika Hospitali ya Muhimbili tumepeleka shilingi bilioni 4.5 na mwaka huu tuna shilingi bilioni 5 lakini kwa JKCI tumeshawapatia shilingi bilioni 1.2.

Mheshimiwa Spika, katika hili, nisema tu kwamba sisi kama sekta ya afya tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutuwezesha kufanya vizuri katika utoaji wa huduma za matibabu ya kibingwa. Nimemshangaa sana Mheshimiwa Sugu anaposema rufaa zimepungua kwa sababu watu wanaogopa kuandika rufaa.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe takwimu chache. Mwaka 2014, Hospitali ya Jakaya Kikwete ilikuwa inafanya upasuaji wa kifua wagonjwa 127. Kutokana na kazi nzuri ya Magufuli mwaka 2017 wamefanyia wagonjwa 275. Sasa tunataka tuwapeleke wapi kama huduma zinapatikana ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala la upasuaji wa moyo bila kupasua kifua mwaka 2018 uwezo wa Jakaya Kikwete ulikuwa ni wagonjwa 100 tu, mwaka 2017 tumefanyia wagonjwa 770. Sasa tunapeleka nje kwa sababu gani? Huduma zimeboreka na Mheshimiwa Sugu anatakiwa ku- appreciate kwamba tunafanya renal transplant na tunafanya upandikizaji wa vifaa vya kusikia kwa watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nitoe mfano wa mwisho, hospitali yetu ya Ocean Road, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais tumepata shilingi bilioni 9.4, tumenunua mitambo ya kisasa ya kutoa matibabu ya mionzi inaitwa LINAC. Kwa kipindi cha miezi mitatu, tumewafanyia wagonjwa 109 na kati ya hao wagonjwa 70 wote tungewapeleka India kwa kila mmoja shilingi milioni 50. Kwa hiyo, wenzetu mnatakiwa kukubali kwamba huduma za matibabu ya kibingwa chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli zimeboreka sana na ndiyo maana safari za India zimepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la fedha, Kamati inasema hatujapokea fedha za miradi ya maendeleo, nadhani tu ni takwimu lakini sisi hadi Desemba tumeshapokea shilingi bilioni 81 kwa ajili ya miradi ya maendeleo ikiwemo fedha za dawa na ndiyo maana hali ya upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutoa huduma za afya ngazi ya msingi na rufaa ni zaidi ya asilimia 90. Pia tumepokea fedha kwa ajili ya kujenga Hospitali za Rufaa za Mikoa katika Mikoa mipya ya Simiyu, Katavi, Njombe, Songwe na Geita. Kwa hiyo, tumepata hela za miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalize kwa suala la viwanda vya dawa au uzalishaji wa ndani wa dawa. Suala hili ni la kipaumbele kwa Serikali na kwa Wizara ya Afya. Nafurahi kusema sasa hivi viwanda vinne vinajengwa na sekta binafsi. Tunacho Kiwanda cha Dawa Bahari, Kairuki Pharmaceutical naye anajenga kiwanda lakini pia Reginald Mengi naye anajenga kiwanda cha dawa na sasa hivi tumepata mwekezaji mwingine ambaye ataanza kujenga kiwanda cha dawa. Kwa hiyo, tunaamini kabla ya mwaka 2020 tutakuwa angalau tuna viwanda vinne vipya ambavyo vinazalisha dawa ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho ni la watumishi lakini naamini kaka yangu Mheshimiwa Mkuchika atalijibu lakini nakubaliana na maoni na ushauri wa Kamati kwamba sasa tuwekeze kuhakikisha vituo vya afya viliboreshwa vinafanya kazi na siyo kuwa na majengo ambayo yanaweza yakamalizwa kwa sababu ya popo. Kwa hiyo, kwenye hili, kipaumbele chetu sisi tunataka kutoka kwenye bora huduma twende kwenye ubora wa huduma. Kwa hiyo, suala la huduma bora za afya ndiyo kitakuwa kipaumbele chetu kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, niseme tena naishukuru na kuipongeza Kamati na kwa kweli Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii ina watu vichwa sana na tunawashukuru sana na naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa fursa, lakini kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuleta hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri. Katika hatua hii napenda kusema kuwa tumepokea maoni yenu na ushauri wenu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya afya, masuala makubwa ambayo yamejitokeza katika michango na maoni ya Waheshimiwa Wabunge, kwanza ni suala la miundombinu ya utoaji wa huduma za afya na ni suala linalohusu ujenzi wa zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya, hospitali za mikoa kwa mikoa ile mitano mipya, lakini pia na hospitali za kanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwepo na suala la rasilimali watu na hili linahusika kwa kiasi fulani na uhaba wa madaktari, wahudumu, wauguzi na wafanyakazi wengine katika sekta ya afya. Lilikuwepo pia suala la upatikanaji wa dawa, vifaa, vifaa tiba na kwa upande wa sekta ya maendeleo jamii, jinsia na watoto, masuala makubwa matatu ambayo yamejitokeza katika mjadala huu ni suala la kuwawezesha wanawake kiuchumi. Pia suala la elimu kwa watoto wa kike na suala la mainstream gender katika mipango yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge wote kwamba katika suala la miundombinu ya huduma ya afya, tutajenga zahanati katika kila kijiji kama tulivyoahidi, tutaonesha katika bajeti yetu, ni zahanati ngapi tutajenga katika mwaka wa fedha 2016/2017; tutaonyesha ni vituo vya afya vingapi vitajengwa na Hospitali za Wilaya ngapi zitajengwa. Tutashirikiana na wenzetu wa TAMISEMI kuhakikisha kwamba 2020 tunaporudi kuomba kura, Watanzania watatupa kura kwa sababu ya ahadi ya kuboresha miundombinu ya vituo vya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la rasilimali watu juzi niliongea. Tunao uhaba wa wafanyakazi especially madaktari katika vituo vyetu vya afya kuanzia ngazi zote, uhaba ni karibu 52%. Kwa hiyo, bajeti inayokuja ya mwaka 2016/2017, tutajikita katika kuajiri watumishi wapya wa sekta ya afya, Mmadaktari, wauguzi na wakunga lakini pia tutaweka kipaumbele katika ile Mikoa tisa kama nilivyosema ambayo ina uhaba mkubwa ikiwemo Katavi, Geita, Simiyu, Tabora na Njombe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo tutalipa kipaumbele ni kuhakikisha kwamba tunatoa motisha kwa Madaktari kukubali kufanya kazi vijijini. Kwa hiyo, tutahakikisha tunajenga nyumba za madaktari, lakini pia tunataka sasa hivi daktari yeyote ambaye anataka kuongeza ujuzi kwa kutumia fedha za Serikali tutampa mkataba, ata-sign mkataba kwamba atakaporudi atakwenda kufanya kazi Katavi kwa miaka mitatu kabla hajaamua kuondoka katika Serikali, hili linawezekana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la vifo vya akinamama wajawazito. Mimi ni mwanamke na nimepewa jukumu hili, nakubali ni changamoto kuona wanawake karibu 7,900 wanafariki kila mwaka kwa sababu tu wanatimiza haki yao ya uzazi. Kila saa moja tulilokaa hapa mwanamke mmoja wa Tanzania anafariki kwa sababu tu anatimiza haki yake ya msingi ya kuzaa. Nimedhamiria, tumedhamiria Wizarani hili suala tutalipa kipaumbele kuhakikisha vituo vya afya vyote vinakuwa na vifaa vya kufanyia upasuaji mdogo, maana wanawake wengi wanakufa kwa sababu wanakosa upasuaji, lakini suala la damu salama, suala pia la kuhakikisha kuna ambulance ili wanawake waweze kukimbizwa pale ambapo watapata matatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie suala moja ambalo kwa kweli Mheshimiwa Edward Mwalongo amelizungumzia, vikwazo vya mtoto wa kike katika kupata elimu. Kwa mamlaka niliyopewa namtangaza Mheshimiwa Edward Mwalongo, Mbunge wa Njombe Mjini kuwa shujaa, champion wa haki ya mtoto wa kike kupata elimu kwa mwaka 2016. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutampa tuzo rasmi ya Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii. Kwa mara ya kwanza katika Bunge hili, mwanaume anasimama, anatetea haki ya zana za kujistiri kwa mtoto wa kike. Hili jambo tumelisema, lakini limesemwa na mwanaume kwa kweli tumepata nguvu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Elimu mwanamke, Mheshimiwa Waziri anayehusika na Utumishi ni mwanamke, Mheshimiwa Jenista na mimi, tutalipigania kuhakikisha watoto wa kike wanapata taulo ili waweze kupata haki yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza na mimi niseme naunga mkono hoja. Lakini pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kusimamia vyema raslimali zetu za nchi.

Mheshimiwa Spika, kadiri tunavyosimamia fedha za nchi maana yake tunawekeza pia katika kuboresha huduma za jamii ikiwemo huduma za afya. Nitoe mfano bajeti ya dawa ya Serikali mwaka 2015 ilikuwa shilingi bilioni 24 mwaka 2016 shilingi bilioni 251, mwaka 2017 tunazungumzia takribani shilingi bilioni 269; kwa hiyo kuna watu wanatakiwa waangalie uhusiano wa hatua ambazo tunachukua katika kusimamia raslimali za nchi, lakini pia katika kuboresha huduma za jamii ikiwemo huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupitia jitihada za Mheshimiwa Rais tumeona kwamba kwa mara ya kwanza hakuna Mtanzania mgonjwa atakuwa analala chini kwa sababu tu ya ukosefu wa vitanda au magodoro. Endapo mgonjwa atalala chini ni kwa sababu hospitali au kituo hicho hakina sehemu ya kuweka vitanda au magodoro, hizi zote ni juhudi za Mheshimiwa Rais, Dkt.John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Spika, tumeona kwa mara ya kwanza Mheshimiwa Rais akisambaza vifaa katika halmashauri zote nchini haijawahi kutokea katika historia ya Tanzania. Tumeona kwa mara ya kwanza ambulance zaidi ya 67 Mheshimiwa Rais akizisambaza nchi nzima, haijawahi kutokea katika historia ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba sasa pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kaka yangu Dkt. Mpango na Naibu Waziri, wifi yangu Dkt. Ashatu Kijaji na wataalamu wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri waliyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sekta ya Afya tutanufaika sana na bajeti hii ambayo inapendekezwa. Kwa mfano Suala la kuendelea kutoza ushuru wa forodha wa asilimia 10 katika sukari ya viwandani maana yake ni kwamba tunawekeza katika utengenezaji wa dawa, viwanda vya dawa vinatumia pia sukari ya viwandani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mpango tunakupongeza sana kwa sababu asilimia 80 ya mahitaji yetu ya dawa tunayanunua kutoka nje ya nchi. Kwa hiyo, sasa hivi tunataka kuhakikisha kwamba dawa zinatengenezwa ndani ya Tanzania, hii ni hatua nzuri na tunaipongeza sana.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tunapongeza bajeti hii kwa sababu imefuta ada ya kuanzisha maduka ya dawa. Tumesema MSD haiwezi kuwa na dawa aina zote kwa asilimia 100; kwa hiyo, lazima yawepo maduka binafsi ya dawa. Mheshimiwa Mpango tunakupongeza kwamba umefuta ada ya kuanzisha maduka ya dawa maana yake dawa zitapatikana katika vijiji, katika mitaa yetu na katika makazi yetu. Dawa si biashara, dawa ni huduma tunawapongeza sana Wizara ya Fedha kwa kuliona suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ambalo tunaona sekta ya afya tutanufaika sana na bajeti hii ni suala la kuwatambua rasmi wafanyabiashara wadogo wadogo wamachinga, mama ntilie, maana yake tutakapowatambua ndiyo pia itakuwa rahisi kwetu kuwafikia katika huduma za social security (huduma ya hifadhi ya jamii) na hapa nazungumzia bima ya afya. Endapo wafanyabiashara hawa wadogo tutaweza kuwatambua maana yake pia itakuwa rahisi kwetu sisi kuwafikia na kuwahimiza wajiunge na bima ya afya.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa ya kupata huduma za afya kwa Watanzania ni suala la gharama ya fedha, kwa hiyo tunahimza wananchi wote wajiunge katika mifuko ya bima ya afya ili sasa iwe rahisi kupata dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho ambalo nilitaka kupongeza bajeti hii ni suala pia la kufuta tozo katika mabango ambayo yanaonesha zahanati, sehemu za huduma, vituo vya afya na hospitali, hili ni jambo zuri kwa sababu litakuwa pia ni rahisi kwa wananchi hasa kwa wakati wa dharura kuhakikisha kwamba wanapata huduma za afya kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizi sasa nijikite katika kujibu hoja tatu ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Hoja ya kwanza imeongelewa na Mheshimiwa Lucy Mayenga, naye alikuwa anazungumzia kuhusu utendaji kazi wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, na kwamba kuna kampuni inaitwa Techno Net Scientific Limited ambayo inaingiza kemikali bila kufuata sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru sana Mheshimiwa Lucy Mayenga, tunakubaliana kwamba ndiyo changamoto hii ipo lakini tumeibaini na sasa hivi tayari Mkemia Mkuu wa Serikali anashirikiana na vyombo vingine vya dola kuhakikisha kwamba tunampeleka mahakamani haraka iwezekanavyo Kampuni hii ya Techno Net Scientific ambayo inajihusisha na shughuli za kuhifadhi na kuuza kemikali za viwandani na majumbani wakati usajili wake umeisha toka tarehe 30 Aprili, 2016. Kwa hiyo, Mheshimiwa nikuthibitishie kwamba uchunguzi umekamilika na ndani ya muda mchache tutampeleka mahakamani mhusika.

Mheshimiwa Spika, nitumie Bunge hili kutoa onyo kwa wote wanaojihusisha na kuingiza kemikali za viwandani na majumbani kuhakikisha kwamba wanazingatia sheria.

Mheshimiwa Spika, mwezi wa tisa tulikuja Bungeni tukaleta sheria ya kuibadilisha Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali iwe Mamlaka (Authorty) maana yake ni kutaka kuipa nguvu na uwezo wa kuweza kusimamia shughuli zake mbalimbali ikiwemo kusimamia kemikali za viwandani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Lucy Mayenga nikusihi dada yangu kwamba ndugu yangu tusiifute hii ofisi kwa sababu licha ya kusimamia shughuli za kemikali, lakini pia ina majukumu mengine ya kuhakikisha inasimamia Sheria ya Teknolojia ya Vinasaba, lakini pia inajihusisha na sheria zinazohusika na vilelezo za sampuli katika makosa ya jinai na Mheshimiwa Mwingulu anaitegemea sana katika kukamilisha mashauri mbalimbali ya kijinai ikiwemo Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo limeelezwa na Mheshimiwa Mbunge Aeshi Hilaly ni suala la uvutaji shisha, kwamba je shisha ina madhara gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika,…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile kwa kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja. (Makofi)

Mhesimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kuzungumza na kwa maandishi wakati wa hoja ambayo iko mbele ya Bunge lako Tukufu. Kipekee napenda kumshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba ambaye aliwasilisha maoni na ushauri wa Kamati ya Kudumu ya Bunge kuhusu utekelezaji wa maagizo ya Kamati pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yangu kwa mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuwashukuru Kambi ya Upinzani ingawa mambo mengi yameandikwa kwa kukosa taarifa na takwimu sahihi ya hali ya Sekta ya Afya inavyokwenda mbele toka Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameingia madarakani. Kwa hiyo, nitawajibu hoja zao. Katika hatua hii tunawashukuru kwa kutoa hoja ambazo hazina mashiko ya takwimu sahihi na hali halisi ya utoaji wa huduma za afya nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hotuba yangu kwa kuzungumza na kwa maandishi ambao ni Wabunge 112; kati yao Wabunge 44 wamechangia kwa kuzungumza na Wabunge 59 wamechangia kwa maandishi. Aidha, Waheshimiwa Wabunge tisa walichangia wakati wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge ni nyingi, kwa hiyo, nitashindwa. Haya makaratasi yote ni majibu ya hoja ambazo zimetolewa. Kwa hiyo, nitatoa tu ufafanuzi katika baadhi ya mambo makuu. Naomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba tumepokea maoni na ushauri wenu na tutaufanyia kazi katika kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawashukuru katika hatua hii ya awali kwa pongezi kubwa nyingi ambazo wametupatia mimi, Naibu Waziri pamoja na Watendaji wa Wizara na Katibu Mkuu. Naomba kupitia kwako niwaahidi Waheshimiwa Wabunge wote, pongezi hizi hazitatufanya sisi tukalewa sifa, bali ni chachu ya kufanya kazi vizuri zaidi ili tuweze kuhakikisha huduma bora za afya, maendeleo na ustawi wa jamii zinapatikana kwa Watanzania, lakini hasa wa kipato cha chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia Universal Health Coverage hatuzungumzii tu Bima ya Afya, maana yake kila Mtanzania wa hali yoyote masikini, kipato cha kati, tajiri wa kijijini, wa mjini aweze kupata huduma za afya bila ya kikwazo chochote ikiwemo kikwazo cha fedha. Kwa hiyo, niseme tu kwamba tumepokea ushauri na pongezi lakini tutaendelea kufanya kazi kuhakikisha tunatatua changamoto za Sekta ya Afya katika nchi yetu, kwani tunatambua bila afya hakuna elimu, bila afya hakuna maendeleo, bila afya bora hakuna uchumi na bila afya bora hakuna ulinzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijatoa ufafanuzi, natambua kwamba Kanuni za Bunge zilishatoa pole, lakini kabla sijaendelea, naomba nami kuungana na Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako Tukufu kutoa pole kwa familia ya Dkt. Reginald Mengi ambaye amekuwa mdau mkubwa wa Sekta ya Afya. Kwa hiyo, tunawapa pole familia na tunawaombea Mwenyezi Mungu awape subira na ustahimilivu katika kipindi hiki kigumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni shahidi, Dkt. Mengi amekuwa akitupa nafasi katika vyombo vyake ITV, Radio One, East Africa Radio kutoa Elimu ya Afya kwa Umma kuhusu masuala mbalimbali. Pia ameweza kusaidia watu wenye ulemavu. Kubwa, tutamkumbuka na kum-miss katika Sekta ya Afya kwa sababu alianza kuwekeza kujenga Kiwanda cha Dawa M-Pharmaceuticals Bagamoyo, lakini Mwenyezi Mungu hakupenda ndoto yake iweze kutimia.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, sasa niruhusu nijibu baadhi ya hoja. Nikianza na hoja ambazo zimetolewa na Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii; tumepokea ushauri na maoni ya Kamati na kwa kweli yote tutayafanyia kazi. Jambo kubwa ambalo walilitolea maoni ni kwamba Serikali ihakikishe fedha zilizotengwa kwa Mwaka 2018/2019 zinatolewa zote na kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakubaliana na ushauri huu na niwaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba tutaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango ili kuhakikisha kwamba fedha zote ambazo zimetengwa katika bajeti ambayo inaisha Juni zinatolewa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninazo habari njema. Mheshimiwa Dkt. Mpango na timu yako ninakushukuru sana. Katika mwezi wa Pili ambapo tulishatoka kwenye Kamati, tumepata shilingi bilioni 62 kutoka Hazina, shillingi bilioni 20 tumepata kwa ajili ya dawa; shilingi billioni 32 tumepewa baada ya kuwa tumeshawasilisha makadirio yetu kwenye Kamati ambazo zitatumika kwa ajili ya kuboresha huduma za matibabu ya kibingwa ikiwemo upandikizaji wa kutumia chembe chembe za mwili tunaita bone marrow transplant.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumepata kutoka Hazina shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kuboresha huduma katika Hospitali za Rufaa za Mikoa. Nje ya bajeti ambayo ilipitishwa na Bunge lako Tukufu Mheshimiwa Oscar Mukasa amesema hapa, sisi pia; mimi na Naibu Waziri na Katibu Mkuu, tunahangaika kutafuta vyanzo vingine vya fedha. Kwa hiyo, nje ya bajeti ambayo imetolewa, ndani ya mwezi wa Nne tumepata shilingi bilioni 58 kupitia Mfuko wa Pamoja wa Afya ambao tumepeleka katika zahanati, katika hospitali za wilaya, katika vituo vya afya kwa ajili ya fedha za uendeshaji. Kwa hiyo, tunapokea maoni na ushauri wa Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ni Serikali ya kushughulikia na kutatua changamoto za watu hasa wanyonge na ndiyo maana fedha hizi zimeendelea kutoka kwa ajili ya kuboresha huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo limeelezwa na Kamati ni kwamba Serikali ikamilishe mchakato wa kuwasilisha Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya. Tunakubaliana na ushauri huu na tunaamini, kama tulivyoahidi katika hotuba yangu, mwezi wa Tisa tutakuja Bungeni kwa ajili ya kuleta mapendekezo ya Sheria ya Bima ya Afya ambayo itamlazimu kila Mtanzania sasa kuwa na Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na hoja za Waheshimiwa Wabunge. Mtanzania masikini kama huna hela ni changamoto kupata matibabu. Tukiangalia takwimu ambazo nimezionesha katika kila Watanzania 100 ni Watanzania nane tu ndio wana Bima ya Afya ya NHIF. Sasa Mtanzania huyo awe na tatizo amezungumza kaka yangu Mheshimiwa Khatib kutoka Pemba, unatakiwa kufanya dialysis session moja ni shilingi 180,000/= mpaka shilingi 250,000/=.

Mheshimiwa Naibu Spika, Daktari anaweza akakwambia ufanye dialysis, yaani kuchuja damu sijui kusafisha damu au kutakasa damu (sijui dialysis kwa Kiswahili), Kutakasa damu nadhani kwa Kiswahili kizuri. Anaweza akakuandikia ufanye mara tatu; minimum anaweza kukwambia ufanye mara mbili kwa wiki. Mara mbili Mtanzania gani anaweza ku-afford shilingi 400,000/= kila wiki kwa ajili ya huduma za dialysis?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeoneshwa huduma za kupandikiza figo, kupandikiza vifaa vya kuweza kuwasaidia watoto kusikia, ni Bima ya Afya ndiyo zimefanya hii kazi ya kutoa huduma hizo ambazo zilikuwa zinapatikana kwa shilingi milioni 30 mpaka shilingi milioni 80. Kwa hiyo, tunakubaliana na Waheshimiwa Wabunge kwamba tutaleta Muswada wa Sheria, lakini pia kabla ya kuleta Muswada wa Sheria, tutaendelea pia kufanya uhamasishaji na kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kujiunga na Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo kwamba Watanzania hawana pesa, kuna suala la willingness to pay na affordability to pay. Kwa hiyo, Watanzania wengi bado hawako tayari kulipa Bima ya Afya. Nitumie Bunge lako Tukufu kutoa rai kwa Watanzania. Ule utamadumi tuaojenga kuchangiana harusi, kuchangiana Kitchen Party, tuujenge katika kuchangiana kununua Bima za Afya kwa ajili ya Watanzania masikini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo limeongelewa na Kamati ya Kudumu ya Bunge, jambo la tatu, ni suala la kufanya uboreshaji wa huduma za uzazi katika maeneo mbalimbali. Tunakubaliana na ushauri wa Kamati. Waheshimiwa Wabunge wenyewe ni mashahidi, hata vituo vya afya vinavyoboreshwa na vilivyoboreshwa 352, asili yake ya andiko la vituo hivi ni kuboresha huduma za uzazi, mama na mtoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili tuliona, hivi sisi kama Mawaziri; nilikaa nikasema, hivi mimi Ummy Mwalimu, Waziri mwanamke, sina background ya Udaktari, lakini bado Mheshimiwa Rais ameniamini niongoze Wizara ya Afya, naacha legacy gani kwa Watanzania? Kwa hiyo, nawashukuru sana wataalam wa Wizara, tuliweza tukakaa tukaandika andiko na ndiyo maana sasa tunaboresha vituo vya afya takriban 350. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Jafo na timu yake kwa sababu walijiongeza na Dkt. Chaula. Sisi tungeweza tu tukatafuta fedha, lakini wao wakaja na wazo la Force Account ambalo limeleta mafanikio makubwa katika uboreshaji wa miundombinu ya afya. Kwa hiyo, tunakubaliana na maoni ya Kamati. Tutaendelea kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nataka kusema mbele ya Bunge lako Tukufu, tunataka Watanzania hasa wanawake ambao ndio wapigakura wa chama changu Chama cha Mapinduzi kujionea kwamba huduma za afya ya mama na mtoto zimeboreka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na vituo vya afya, pia tumeanzisha kampeni mbalimbali za kuhamasisha uwajibikaji na matokeo chanya katika kupunguza vifo vya akina mama na mtoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, ambaye amekuwa ndio mlezi wa kampeni hii. Tumeweza pia kuhakikisha tunaweka wataalam wakiwemo wataalam wa kutoa dawa ya ganzi na usingizi ambapo tumeweza kugharamia mafunzo takriban ya watu 200.

Mheshimiwa Naibu Spika, wifi yangu, sijui kama naruhusiwa kusema hivyo, Mheshimiwa Esther Matiko nitamjibu baadaye, lakini anaweza akasema labda tunasema. Ukitaka kupima, je, tunakwenda mbele katika eneo hili la afya ya mama na mtoto au hatuendi mbele? Tunaangalia viashiria vikuu ambavyo vimewekwa na Shirika la Afya Duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiashiria cha kwanza: Je, huduma za uzazi wa mpango zinaendelea? Kwa mujibu wa takwimu zetu, tumeongeza kiwango cha watumiaji wa huduma za uzazi wa mpango kutoka asilimia 32 hadi asilimia 38. Hizi ni takwimu za NBS. Tukiangalia program data tutakuwa tuko vizuri zaidi.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Huo ndiyo ukweli.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, wakati wenu wa kuchangia Mheshimiwa Waziri alikuwa kimya akiwasikiliza na ninyi msikilizeni anapowajibu. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, huo ndiyo ukweli. Hata tukiangalia akina mama wanaojifungulia katika vituo vya kutoa huduma za afya, kabla Mheshimiwa Dkt. Magufuli hajaingia madarakani ilikuwa ni asilimia 65 lakini kwa sababu huduma za uzazi za mama na mtoto zimeboreka, tumeongeza idadi ya akina mama wanaojifungua katika vituo vya kutoa huduma za afya kufikia asilimia 32. Huu ndiyo ukweli, hata katika ngazi ya mikoa, inaonekana kwamba hali ya huduma za mama na mtoto zinaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ambalo ndiyo viashiria vikuu vya afya ya uzazi ya mama na mtoto, je, kuna ongezeko la akina mama wajawazito ambao wanahudhuria kliniki angalau mara nne katika kipindi cha ujauzito wao. Tumeonyesha pia kwamba lipo ongezeko la zaidi ya asilimia 30 la wanawake ambao wanahudhuria kiliniki angalau mara nne. Kwa hiyo, hivi ndiyo viashiria vikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunakuja kwenye takwimu, je, vifo vimepungua au havijapungua. Utafiti uliofanywa na Taasisi ya Takwimu ya Taifa (NBS), ulikuwa ni utafiti wa mwaka 2015, kwa hiyo, sasa hivi hatuna takwimu zaidi ya hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, nasimama mbele ya Bunge lako Tukufu, NBS akifanya utafiti mwingine, sina shaka, vifo vya akina mama wajawazito vitakuwa vimepungua kwa zaidi ya asilimia 50. Tukikusanya takwimu ambazo tunazo katika mikoa, sipendi kuzitaja kwa sababu siyo takwimu rasmi, lakini hali inaonyesha kwamba tumepunguza kwa kiasi kikubwa vifo vya akina mama wajawazito. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya nne ambayo imeelezwa na Kamati na ambayo tumeipokea ni suala la maambukizi ya UKIMWI na kwamba katika maambukizi mapya ya UKIMWI asilimia 44.6 ni vijana wakati sheria inakataza mtu mwenye umri wa miaka 18 kupima UKIMWI bila ya ridhaa ya wazazi lakini pia inakataza mtu kujipima UKIMWI mwenyewe isipokuwa apime katika vituo vya kutolea huduma za afya. Tumepokea ushauri na tayari tumeandaa marekebisho ya Sheria ya VVU na UKIMWI, Sura ya 431 ambayo tumependekeza turuhusu mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 18 kupima UKIMWI bila kuhitaji ridhaa ya mzazi au mlezi. Pia tunapendekeza kwamba tutafanya marekebisho ya sheria hiyo, kifungu 13(4) ili kuondoa ulazima wa watu kupima VVU katika vituo vya kutolea huduma za afya tu. Kwa hiyo, hayo tunategemea kuja katika Bunge lako Tukufu mwezi Septemba ili tuweze kufanya marekebisho haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Kamati kwamba hatuwezi kufikisha lengo la pili na la tatu la kuhakikisha tunatokomeza UKIMWI kama hatutatimiza lengo la kwanza ambalo sasa hivi takwimu rasmi za NBS zinaonyesha kwamba ni asilimia 51. Takwimu rasmi za programu data tunaonyesha kwamba watu ambao wanaishi na Virusi vya UKIMWI na wanajua hali yao ni asilimia 75. Kwa hiyo, sina shaka kwamba tukifanya haya marekebisho mawili ya kuruhusu watu kujipima UKIMWI na watoto kuruhusiwa kujipima bila ridhaa ya wazazi/walezi kwa sababu wanaolewa kwenye miaka 15 au 16 tutaweza kuongeza kasi ya kupambana na UKIMWI.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tano ambalo limeongelewa na Kamati ni suala la afya ya usafi na mazingira kwamba tushirikiane na Wizara ya Maji, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Tumepokea yote haya na ni kweli nikiwa kama Waziri ambaye nasimamia sekta ya afya, tunaona mzigo mkubwa wa wagonjwa, takribani katika kila wagonjwa 100 wanaohudhuria OPD kwa maana ya wagonjwa wasio wa kulazwa asilimia 60 ni magonjwa haya yanayotokana na suala zima la usafi. Pia tuna taarifa ya Benki ya Dunia ambayo imeonesha kwamba Tanzania tunapoteza takriban shilingi bilioni 400 kila mwaka kutokana na hali duni ya usafi. Kwa hiyo, tumepokea ushauri kuhusiana na hali duni ya usafi na tutayafanyia kazi masuala haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la sita ambalo limezungumzwa na Kamati kwa upande wa Fungu 52 ni huduma za lishe. Tunalipokea na sisi tutaendelea kuhamasisha wananchi kuhakikisha kwamba wanazingatia lishe bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende katika hoja zilizoletwa na Kamati kwa upande wa Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii na kubwa lilikuwa Serikali ihakikishe kwamba Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii inatengewa fedha kwa ajili ya kufanya kazi za maendeleo na ustawi wa jamii. Tumepokea ushauri huu na naamini Mheshimiwa Dkt. Mpango ananisikia kwamba Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii nao wana mchango mkubwa katika kuhakikisha tunajenga Tanzania ya Uchumi wa Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge, hata juzi nimeongea na Watendaji wa Wizara, Wizara hii ni moja, kwa hiyo, lazima sasa tuoneshe kwamba hakuna Vote ya Maendeleo ya Jamii ya Jamii au Vote ya Afya, bali ni Wizara moja. Kwa hiyo, tunaona Sekta ya Afya inapata rasilimali nyingi kutoka kwa wadau, kwa hiyo, tumeamua tutakuwa tunakata asimilia ya fedha za wadau ambazo tunazipata kwenye Sekta ya Afya, tutazipeleka kwenye Sekta ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala kubwa ambalo lilitolewa sasa na Hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani. Kuna jambo moja naomba niliseme, hii hotuba ukisoma, kuna maneno mengine unasema, hivi huyu ni Mtanzania ambaye yuko Tanzania au yuko nje ya nchi, anazungumza mambo ambayo hajui nini kinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mtu anasema, anasema majigambo ya Serikali kwamba imeboresha sekta ya afya nchini ni kutafuta umaarufu wa kisiasa. Hivi unajiuliza hivi huyu, anajua analolisema au basi tu anataka kusema ili aweze kusikika anaposema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, binadamu mwema ni yule mwenye kushukuru, lakini pia kazi kubwa imefanyika chini ya Utawala wa Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Esther Matiko, shida iko wapi Mheshimiwa Esther Matiko tafadhali, hajakutaja wewe anaongea kwenye hotuba, kwa nini usimpe muda azungumze amalize, kwa nini usimpe nafasi azungumze? Tafadhali Mheshimiwa Esther Matiko, hii ni mara ya mwisho nakutaja jina humu ndani, tafadhali. Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema huduma za afya zimeboreka hatutafuti umaarufu wa kisiasa, bali ndiyo ukweli. Naomba nitoe mifano kama minne, wakati Mheshimiwa Dkt. Magufuli anaingia madarakani, watoto waliokuwa wanapata chanjo ni chini ya asilimia 85, leo asilimia 99 ya watoto wote wenye umri wa chini ya mwaka mmoja wanapata chanjo na nieleze ni halmashauri gani imekosa chanjo za watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati naingia, wazazi wamejifungua watoto hawana chanjo za kuwazuia na kifaduro, kifua kikuu, leo chanjo zinapatikana za watoto katika kila watoto 100, watoto 99 wanapata chanjo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika huduma za matibabu ya kibingwa, Wabunge wameona, kabla Mheshimiwa Dkt. Magufuli hajaingia madarakani, niambieni kama kulikuwa na upandikizaji wa figo, niambieni kama kulikuwa na upandikizaji wa vifaa vya kuweza kusikia, lakini leo hadi ninaposema kuanzia mwaka 2017, Watanzania 38 wameweza kupandikiziwa figo katika Hospitali yetu ya Taifa Muhimbili; Watanzania saba wameweza kupandikiziwa figo katika Hospitali yetu ya Benjamin Mkapa. Hawa Watanzania, hawawezi kusema ni umaarufu wa kisiasa, ila wanamshukuru Mheshimiwa Rais kwa sababu amewezesha huduma hizi kupatikana na zingekuwa zinapatikana nje ya nchi, wasingeweza kutoa milioni 100, milioni 120 kupata huduma hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cochlear implant, upandikizaji watoto wa vifaa vya kuwasaidia kusikia, havijawahi kufanyika, vimefanyika wakati wa Mheshimiwa Dkt. Magufuli, watoto 21 wamefanyiwa. Sasa unajiuliza, hivi huyu anaposema ni umaarufu wa kisiasa, nadhani tumsamehe bure. Hivi anaposema ni umaarufu wa kisiasa, anaandika kwenye speech, umaarufu wa kisiasa, watoto 21 wamepandikizwa vifaa vya kuwasaidia kusikia! cochlear

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kutoa mifano, health centers, vituo vya afya 352 vinaboreshwa na vimekamilika, tuna Hospitali za Wilaya 67 zinaendelea kujengwa, lakini pamoja na msomaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani, ana Kituo cha Afya kinaitwa Magena kimepata milioni 400. Halafu atasema ni umaarufu wa kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kusema, yapo mambo makubwa ambayo yamefanywa na Serikali ya Awamu ya Tano na kwa kiasi kikubwa huduma za afya zimeboreshwa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kukiri kwamba, changamoto za afya bado ni nyingi na tutaendelea kuzifanyia kazi, lakini lazima tushukuru mambo makubwa na mazuri ambayo yamefanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tena nimalize, suala la pili, ambalo Kambi Rasmi ya Upinzani imehoji, kwamba bajeti ya afya imepungua kutoka shilingi trilioni moja hadi shilingi bilioni 866, lakini pia tunategemea fedha za wazungu. Kwa hiyo, hawa hawa Wabunge ndiyo wamekuwa wakituambia tupunguze utegemezi wa wahisani! Kwa hiyo, kilichopungua, Mheshimiwa Dkt. Mpango ni shahidi, tumepunguza fedha zilizotoka kwa wahisani, lakini fedha za ndani ya nchi, fedha za walipa kodi wa Tanzania, zimeendelea kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia bajeti ya mwaka 2017/18 ilikuwa bilioni 628, lakini mwaka 2018/2019 bilioni 681; mwaka 2019/2020 bilioni 686.6, kwa hiyo, unaziona fedha za ndani zinaendelea kukua, lakini ni kweli fedha za nje tumepunguza! Tulianza mwaka 2017/2018 ilikuwa ni bilioni 449, tumepunguza mpaka bilioni 184 na mwaka huu tunaomba fedha za nje bilioni 272. Kwa hiyo, inategemea unaliangalia kwa perspective gani, lakini kama ni kuongeza fedha za ndani, hakuna fedha ya afya ambayo imepungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna swali pia limezungumzwa na Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu suala la PPP, hilo sisi niseme tulishaanza kulifanyia kazi na kwa mfano katika kufunga mashine za kupima maambukizi ya damu, tumeweza pia kuingia mikataba na mdau ambaye amefunga mashine hatutumii fedha za Serikali, lakini pia tumetangaza tenda ya kuweza kuhakikisha tunafunga vifaatiba bila kutumia fedha za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo limeelezwa na Kambi Rasmi ya Upinzani ni suala la huduma ya afya bila malipo kwa wanawake, lakini pia tumewasikia, suala la Wakunga wa Jadi kwamba wamezuiliwa. Tulichokitaka, siyo kuwazuia Wakunga wa Jadi, tunaendelea kutambua na kuthamini mchango wa Wakunga wa Jadi kama wadau wakubwa wa huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto. Sasa tunachokifanya, tunataka hawa watu wawe kama ni daraja letu kati ya vituo vya kutoa huduma za afya pamoja na Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunasema kwamba Wizara itaendelea kuwaelimisha Wakunga wa Jadi kuhusu umuhimu wa kuwashauri wajawazito kwenda katika vituo vya kutolea huduma mapema ili kupata huduma bora na salama za kujifungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani hayo ndiyo makubwa ambayo ningetaka kuyajibu kutoka kwenye Kambi Rasmi ya Upinzani, lakini mengine yote tunakubaliana na wao, ikiwemo kuendelea, kuhakikisha tunatumia Community Health Workers, amezungumza Mheshimiwa Kandege kwamba changamoto ambayo tunaipata na kuna baadhi ya Wabunge wametoa mfano, kuna vituo vya afya vinaongozwa na Medical Attendant (Mhudumu wa Afya), lakini kuna vituo vya afya unakuta vinaongozwa na Wauguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo sasa ndiyo tunajaribu kuweka balance, uwiano. Je, tujaze watumishi wa kwenye facilities au twende kwenye Community Health Worker, lakini as a matter of sera, ikiwa ni suala la kimsingi, tunakubaliana nalo na especially mimi katika ajenda yetu ya kuhakikisha tunaongeza hali ya lishe kwa akinamama wajawazito na watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano, lakini pia tunaongeza watu ambao wanajua maambukizi ya Virusi vya UKIMWI na katika mapambano ya kifua kikuu tunaamini kwamba wahudumu wa afya ngazi ya jamii watato mchango mkubwa. Tunategemea kuajiri takriban 600 kupitia fedha ya Mfuko wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja zilizoelezwa ni nyingi, ikiwemo uboreshaji wa huduma katika ngazi zote tumepokea na lengo letu kwa kweli tunataka kutoka kwenye bora huduma twende huduma bora na ndiyo maana Wizara ya Afya tunayo idara ya kusimamia uhakiki wa ubora wa huduma za afya. Kwa hiyo, tutahakikisha kinafanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunakusudia kutoa usajili wa vituo vya kutoa huduma za afya vya Serikali na binafsi. Lengo letu tukiona, hata cha Serikali tukikiona hakina ubora, tunataka kukifungia kama vile tunavyofungia vituo vya afya vya binafsi. Kwa hiyo, hili ni eneo ambalo tumekubaliana kwamba tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la vifaa na vifaatiba kwa ajili ya vituo vya afya vilivyoboresha, Mheshimiwa Naibu Waziri ameongea kwamba tumeanza kununua lakini tutahakikisha kwamba, kwa sababu hata zoezi hili la kukarabati vituo vya afya, lilienda kwa awamu, kwa hiyo niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba tutahakikisha tunanunua vifaatiba na kuvifunga katika vituo vya afya vilivyoboreshwa ili viweze kutoa huduma bora zilizokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lilikuwa wazo, hoja ambazo pia zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge ni suala la X-Ray machines; wengi wameeleza kwamba hazifanyi kazi au ni za zamani. Naendelea kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba tumeshaagiza x-rays takriban 70 za kisasa, kwa hiyo, tutazisambaza katika Hosptali za Rufaa za Mikoa, lakini pia katika Vituo vya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mzee wangu Deo Sanga, nimemsikia kuhusu Makambako, nakubaliana na yeye, hata kama ni kituo cha afya, kwa kweli tutahakikisha kwamba anapata x-ray ili kuweza kutoa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kumezungumzwa suala la ambulance, Waheshimiwa Wabunge tumewasikia sana na tulikuwa tunaongea na Mheshimiwa Waziri Mkuu hapa, mahitaji ya ambulance ni mengi, lakini kama nilivyoeleza katika hotuba yangu, tayari tumeagiza ambulances 50, kwa hiyo tutazigawa katika maeneo yenye uhitaji, lakini tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kugawa ambulance.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijamaliza, nizungumzie suala ambalo pia limeongelewa na Waheshimiwa Wabunge, kwamba maiti anachajiwa, anadaiwa sijui. Kwa kweli, tunapata changamoto, lakini naomba Waheshimiwa Wabunge watuelewe, angalau katika Tanzania na hasa Hospitali yetu ya Taifa Muhimbili, kipaumbele wanakiweka kwa mgonjwa kupata huduma. Maana bora mtu angekufa kwamba kakosa huduma, lakini mtu kwanza anapata huduma, akishapata huduma ndiyo linakuja suala la deni. Nilikuwa naongea na Profesa Museru, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali yetu ya Taifa, Muhimbili, amenieleza, Mheshimiwa Waziri ambao wanakuja kwako pia, saa nyingine hawafuati taratibu. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Watanzania, kwanza kuhakikisha tunawekeza kwenye afya zetu kwa kukata bima ya afya, lakini pale ambapo hatuna uwezo wa kulipia, basi tufuate utaratibu wa kupata matibabu bila malipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninazo takwimu hapa, tukiangalia Hospitali ya Taifa Muhimbili, kuanzia Julai mpaka Disemba, iliweza kutoa msamaha kwa wagonjwa wenye thamani ya shilingi bilioni 2.7, kwa hiyo, watu wanasamehewa. Vile vile tukiangalia Hospitali ya MOI, Julai hadi Desemba, ilitoa msamaha kwa wagonjwa wenye thamani ya shilingi milioni 347. Tukiangalia Mloganzila Julai hadi Desemba, 2018 walitoa msamaha kwa wagonjwa wenye thamani ya shilingi milioni 178.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninazo takwimu mpaka za Hospitali zetu za Rufaa za Mikoa, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge tunaomba watuelewe, hapo hapo tunahitaji kuboresha huduma, sasa tukisema tu jamani kila kitu bure bure bure, jamani bure, bure ni gharama, bure ni gharama.

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia tena bure ni gharama, kwa hiyo muhimu tuendelee kuhakikisha kwamba, kwanza tunawekeza kwenye afya zetu, lakini pili pia tunafuata taratibu katika kupata huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumze suala moja ambalo limeongelewa na Mheshimiwa dada yangu Taska Mbogo, kuhusu Customary Declaration Order, ni ya zamani na kandamizi na inabagua wanawake. Nakubaliana sana na Mheshimiwa Mbogo, kwamba sheria hii ni ya zamani, lakini kuna maamuzi ya Mahakama Kuu kwenye Kesi Na. 82 ya mwaka 2005 ambayo inatambulikana kama Elizabeth Stephen na mwenzake dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ambayo ilitolewa maamuzi tarehe 8 Mwezi wa Tisa mwaka 2006, mbele ya Majaji watatu wa Mahakama Kuu kuwa, Serikali imeweka kifungu cha 12 cha Sheria ya Judicature and Application of Laws Act, ambacho kinamtaka mtu yeyote atakayeona kuna mila kandamizi inayomzuia kupata haki yake, kufuata utaratibu uliowekwa katika kifungu hicho kwa kuwasilisha maombi ya kubatilisha mila hiyo kupitia Waziri wa TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba kusema hii ni changamoto. Dada yangu Mheshimiwa Taska Mbogo, naomba nilichukue, tutakwenda kulifanyia kazi ili kuhakikisha ikiwezekana tunafuta sheria hii. Kwa sababu hoja ambayo ipo ni kwamba kuna baadhi ya mila zetu ambazo zimo ndani ya sheria hii siyo mbaya, za kutunza wazee na watoto wa ndugu. Kwa hiyo, tutaangalie yale ambayo yanamkandamiza mwanamke tutaweza kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mdogo wangu Mheshimiwa Amina Mollel amezungumzia suala la unyanyasaji wa wasichana hasa wanaosoma katika vyuo vya elimu ya juu. Sera ya Usawa wa Jinsia na Maendeleo ya Wanawake inahimiza kuanzishwa kwa Madawati ya Jinsia katika Taasisi, Wizara na Idara za Serikali. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuvitaka vyuo vya elimu ya juu nchini kuanzisha Madawati ya Jinsia ili kuweza kushughulikia changamoto mbalimbali za jinsia ikiwemo vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya wanafunzi katika vyuo vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipongeze sana jitihada za Kamishna Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ambaye ameanzisha Dawati la Jinsia ndani ya TAKUKURU ili kuweza kupambana na rushwa ya ngono. Kwa hiyo, nitoe pia wito kwa wanafunzi wa vyuo vya elimu juu ambao wananyanyaswa au wanakumbana na vitendo vya ukatili wa kijinsia kuhakikisha kwamba wanatoa taarifa katika Dawati hili la Jinsia ambalo limeanzishwa mwaka huu chini ya TAKUKURU.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, hoja ambazo zimeongelewa ni nyingi lakini kipekee niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge wa kutoka Mikoa mipya ya Katavi, Songwe, Njombe, Simiyu na Geita kwamba kipaumbele chetu kama Wizara tumekubaliana mwaka huu ni kukamilisha Hospitali za Rufaa za Mikoa ili ziweze kutoa huduma za rufaa katika mikoa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika Mkoa wa Singida na Shinyanga, mdogo wangu Mheshimiwa Aisharose Matembe na ndugu yangu Mheshimiwa Azza Hillal, kama Wizara tumejipanga kuhakikisha tunakamilisha ujenzi wa Hospitali za Rufaa za Mikoa. Lengo ni ili sasa tuweze kukabidhi Hospitali ya Shinyanga kwa Manispaa ya Shinyanga, pia tukabidhi Hospitali ya Singida kwa Manispaa ya Singida. Kwa hiyo, mdogo wangu Mheshimiwa Aisharose na ndugu yangu Mheshimiwa Azza Hillal tunataka kuwathibitishia kwamba jambo hili pia tutalikamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika hospitali nyingine za Rufaa za Mikoa kama tulivyosema tumezipokea kuanzia tarehe 1 Julai 2018. Tunachokifanya, tumeamua kuwekeza katika maeneo makubwa manne. Eneo la kwanza ni kuhakikisha tunakuwa na miundombinu ya kutoa huduma kwa wagonjwa wa dharura na ajali (emergence medicine) na tayari tumeanza kupata fedha kutoka Global Fund tutaanza kuweka vitengo vya dharura katika hospitali saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni kuweka huduma za ICU, huduma kwa wagonjwa wanaotaka uangalizi maalum. Huduma hii tutafanya pia katika hospitali zote za Rufaa za Mikoa. Eneo la tatu ni kuboresha huduma za uzazi. Eneo la nne tunataka kuhakikisha tunaweka Madaktari Bingwa katika Hospitali za Rufaa za Mikoa yote. Tumebainisha maeneo nane ya kipaumbele, tunataka kuhakikisha tuna Madaktari Bingwa wa magonjwa ya uzazi na wanawake angalau wawili, magonjwa ya watoto angalau wawili, upasuaji angalau wawili, upasuaji wa mifupa angalau wawili, usingizi na radiolojia na magonjwa ya ndani (internal medicine).

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hayo ni maeneo ambayo tumeyabainisha na tutahakikisha kwamba kila Hospitali za Rufaa za Mikoa zinakuwa na wataalam hawa. Kama alivyosema Naibu Waziri tayari tumeanza kusomesha madaktari na ili tuweze kukupa ufadhili wa kusoma masters ya udaktari tutawafungisha mkataba ili wakimaliza waweze kufanya kazi katika Hospitali zetu za Rufaa za Mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema mambo ni mengi lakini kwa kweli kipee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, asiye na macho haambiwi tazama, kazi kubwa na nzuri imefanyika katika utoaji wahuduma za afya. Mimi niseme tutaendelea kuhakikisha tunatimiza ndoto yake ya kuifanya Tanzania ya viwanda kwa kuboresha huduma za afya kwa kuhakikisha kwamba Watanzania wanakuwa na afya bora badala ya kusubiri kwenye mambo ya tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge tumewasikia, Mzee wangu Mheshimiwa Lubeleje tumekusikia, tunataka na sisi tuondoke kwenye taifa la kulilia dawa, dawa, lakini liwe ni taifa la kulilia afya na lishe bora. Kwa hiyo, jambo hili pia tutalifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kumshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais, mama Samia Suluhu Hassan ambaye kwa kweli amekuwa akinipa msaada mkubwa katika utekelezaji wa majukumu yangu. Namshukuru sana mama Samia katika kuimarisha afya ya uzazi ya mama na mtoto. Mheshimiwa dada yangu Mariam Kisangi ameonesha, watu wanaosema hakuna mabadiliko, Hospitali ya Mkoa wa Rufaa ya Temeke hakuna kifo kimetokea mwezi Machi, mama Kisangi ni shahidi na watu wanaona. Halafu watu wanasema hakuna kazi imefanyika, kazi imeonekana ndiyo maana hakuna vifo vya akina mama wajawazito.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa uongozi wake mahiri na nawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri wote. Kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile, Naibu Waziri kwa mchango mkubwa sana ambao ananipatia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi niliambiwa unajua hawa madaktari wanaweza wakadharau lakini Naibu Waziri amekuwa akinipa mchango na heshima kubwa katika utendaji wa kazi zangu. Mheshimiwa Naibu Waziri nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimshukuru pia Katibu Mkuu (Afya), Dkt. Zainabu Chaula. Kwa kweli tunafurahi sana kama Wizara ya Afya tumepata mama ambaye anajua kusukuma mambo na anajua kusimamia utendaji katika Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia namshukuru sana Dkt. John Jingu ambaye naye ni Katibu Mkuu, Maendeleo ya Jamiii kwa kazi kubwa na nzuri ambayo amefanya katika kusimamia Sekta ya Maendeleo ya Jamii. Tunamshukuru sana pia Mganga Mkuu wa Serikali na madaktari wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili tunawashukuru madaktari, wauguzi na watoa huduma za afya nchini. Hapa naongea kama Waziri wa Afya, nitoe maelekezo na maagizo kwa viongozi wenzangu, tuache kuingilia fani za kitaaluma. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna daktari au muuguzi amekosea ashughulikiwe kwa mujibu wa taratibu za Utumishi wa Umma. Narudia tena, kama kuna daktari amekosea tuleteeni kwenye Baraza la Madaktari, tutafuta usajili wake. Kama kuna muuguzi amekosa tuleteeni kwenye Baraza la Wauuguzi na Wakunga tutafuta usajili wake. Kama kuna mfamasia amekosea tuleteeni kwenye Baraza la Wafamasia ambalo ndiyo limeanzishwa kisheria kushughulikia changamoto kama hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka mitatu ambayo nimekaa katika sekta ya afya, Naibu Waziri ameongea, kazi ya wauguzi watano inafanywa na muuguzi mmoja halafu bado huwezi ku-appreciate (kuthamini)? Madaktari hawa wanajituma sana, kwa kweli lazima tutambue mchango wao na tuheshimu kazi kazi yao nzuri. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi na Naibu Waziri tutaendelea kuwatetea madaktari na wauguzi wetu kwa sababu mwisho wa siku wanaopata matatizo ni Watanzania wanyonge. Mwenye hela zake haendi kwenye hospitali ya Serikali au kituo cha afya cha Serikali. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli inatia uchungu, sisi ambao tuko kwenye sekta hii tunaelewa changamoto ambazo watoa huduma za afya wanapata. Kwa hiyo, sisemi kwamba wote ni malaika au ni wazuri, hapana, wapo wabaya lakini tufuate taratibu za kuwawajibisha watumishi watoa huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa ushirikiano mkubwa na mzuri ambao wamekuwa wakinipatia katika kutekeleza majukumu yangu. Kipekee, nawashukuru wadau wetu wa maendeleo hususani wanaochangia Mfuko wa Afya wa Pamoja ambao ni Denmark, Canada, KOICA, UNICEF na World Bank, nadhani nimewamaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nawashukuru na wadau wengine ambao hawachangii kwenye Mfuko wa Afya lakini mchango wao ni mkubwa ikiwemo Global Fund, Mfuko wa Rais wa Marekani wa Kupambana na UKIMWI pamoja na watu wa GAVI, Abbott Fund wote hao wanatusaidia, pamoja mashirika yasiyo ya kiserikali na mashirika ya dini. Nawashukuru sana Wakuu wa Taasisi na Idara za Serikali, Hospitali zetu za Taifa Muhimbili, Bugando, Jakaya Kikwete, Ocean Road, MOI, Benjamini Mkapa na hospitali nyingine zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niwaambie Waheshimiwa Wabunge tutajibu hoja zenu zote kwa maandishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, sasa naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kuzipongeza Kamati zetu mbili; Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii inayoongozwa na Mheshimiwa Peter Serukamba na Kamati ya UKIMWI na Madawa ya
Kulevya inayoongozwa na Mheshimiwa Oscar Mukasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba tumepokea maoni na ushauri wa kamati na pia ushauri wa Waheshimiwa Wabunge katika michango yao, lengo letu likiwa ni kuhakikisha kwamba wananchi wanakuwa na afya bora ili kuwawezesha kushiriki katika ujenzi wa Tanzania ya viwanda lakini pia katika kuboresha maisha yao. Kwa kweli tunazipongeza Kamati, wametoa maoni na ushauri mkubwa na kamati hizi zimekuwa msaada mkubwa kwetu sisi Wizara katika kuboresha huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maoni makubwa ambayo yametolewa na Kamati, suala la kwanza ni kwamba tuhakikishe tunaongeza watumishi katika sekta zote mbili; Sekta ya Afya na Sekta ya Maendeleo ya Jamii. Ni kweli tunakubaliana na maoni na ushauri wa Kamati, lakini niseme kwa nini tunao upungufu mkubwa wa Watumishi wa Afya? Ni kwa sababu ya uwekezaji mkubwa ambao tumeufanya wa ujenzi wa Vituo vya Afya, ujenzi wa Hospitali za Wilaya, ujenzi wa Hospitali za Rufaa za Mikoa sita pamoja na Hospitali Maalum. Kwa hiyo, kadri tunavyopanua miundombinu ya kutoa huduma za afya ndivyo mahitaji ya rasilimali watu yanavyohitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme, Wizara yangu pamoja na ya kaka yangu Mheshimiwa Kapt. Mstaafu George Mkuchika, tumekaa tukabainisha mahitaji halisi ya ongezeko la Watumishi wa Afya, tumeandaa mpango wa miaka mitano na tunajua ni kiasi gani tunahitaji ili tuweze sasa kuhakikisha vituo vyetu vyote vya kutoa huduma za afya vinakuwa na watumishi wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejipanga, ikifika mwaka 2022 tupunguze uhaba wa Watumishi wa Afya kutoka asilimia 52 iliyopo hadi asilimia 30. Nami naamini hili jambo linawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile umetoka ushauri wa Waheshimiwa Wabunge kwamba tutumie watumishi wa kujitolea (volunteers); tumeanza katika Hospitali zetu za Rufaa za Mikoa tumeanza katika Hospitali zetu za Kitaifa. Nikitoa mfano, hospitali ya Dodoma, kila mwezi inatumia shilingi milioni 35 kwa ajili ya watumishi wanaojitolea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, changamoto ipo katika Vituo vya Afya na Zahanati, kwa sababu wao hawana makusanyo ya kutosha. Hawa watu watajitolea, wanahitaji posho ya kujikimu, wanahitaji usafiri. Hawawezi wakajitolea watoto wetu bila kuwapa motisha (incentive) ili waweze kutoa huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwathibitishie Kamati na Waheshimiwa Wabunge, kadri tutakavyopata Watumishi wa Afya, tutaweka kipaumbele kwenye huduma za afya ya msingi, kwenye Zahanati, kwenye Vituo vya Afya na Hospitali za Wilaya. Amesema vizuri kaka yangu Mheshimiwa Ndassa (Senator), kadri tutakavyoboresha huku chini, ndivyo tutakapopunguza mzigo katika Hospitali za Rufaa za Mikoa na Hospitali za Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni la ugharamiaji wa huduma za afya (health care financing) na hili limegawanyika katika maeneo makubwa mawili. Kamati inatushauri tuongeze bajeti ya fedha za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, tuseme, suala la afya ni kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli. Serikali ya Awamu ya Tano inajali na kuthamini afya za Watanzania. Kwa sababu ya msingi bila wananchi kuwa na afya bora, hatutaweza kufikia Tanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hata ukiangalia, nadhani kuna sintofahamu; tutofautishe bajeti ya Wizara ya Afya na Bajeti ya Sekta ya Afya. Bajeti ya Sekta ya Afya inapitia pia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, inapitia katika vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ambapo kuna Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali ambao ni Watanzania hawa hawa wanapata pia huduma za afya. Kutokana na jambo hili, Serikali ya Awamu ya Tano tukiiangalia, tumeongeza bajeti ya Sekta ya Afya kutoka shilingi trilioni 1.2 mwaka 2013/2014 hadi shilingi trilioni 1.8 mwaka 2019/2020. Sisemi kwamba fedha hizi zinatosha, lakini unaiona dhamira yetu ya dhati ya kutaka kuboresha huduma za afya. Matokeo chanya yameanza kuonekana, hatujisifii tu kwamba tumejenga majengo nilikuwa Kome kwa rafiki yangu Mheshimiwa Tizeba, mama mjamzito sasa hivi anajifungulia Kome bila ya kuvuka kivuko kwenda Sengerema kujifungua, rafiki yangu Mheshimiwa Allan Kiula Mkalama kituo cha afya mama mjamzito anapata huduma za uzazi za dharura pale pale, kwetu sisi Awamu ya tano haya ni mafanikio makubwa sana ya kuokoa maisha ya mama mjamzito lakini ya kuokoa maisha ya watoto wa changa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge wa Kinondoni Mtulia amesema miaka minne iliyopita tulikuwa tunapeleka wagonjwa zaidi ya 600 kwa mwaka nje ya nchi, kwetu sisi siyo suala la kupunguza gharama sasa hivi tumetoka 600 mpaka 53 maana yake nini? Wananchi wengi zaidi wanapata huduma za upasuaji wa moyo ndani ya nchi, ukipeleka India utapeleka 600 ukifanya ndani ya nchi unafanya zaidi ya watu 3,000; kwa hiyo siyo suala la gharama lakini ni suala la kuhakikisha hata Mtanzania masikini anapata huduma bora za matibabu ya kibingwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwenye hili niahidi kwamba Serikali itaendelea kuongeza bajeti ya sekta ya afya kadri uchumi wetu utakavyoruhusu kwa sababu tunavyo vipaumbele vingi, tunavipaumbele vya maji, tunavipaumbele vya umeme, vya kilimo, lakini tutajitahidi kuongeza kuongeza bajeti kadri hali ya kiuchumi itakavyo ruhusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la ugharamiaji wa huduma za afya, liko suala la wananchi kumudu gharama namshukuru sana Mheshimiwa Mwenyekiti Peter Serukamba na kamati yake kwa mara ya kwanza wameona mzigo mkubwa ya misamaha ambayo hospitali zetu zinabeba. Kwa hiyo tunavyokaa tukalaumu huduma mbaya na sisi ndiyo maana Wizarani tumesema tuje sasa na takwimu, misamaha kwa kila hospitali ni shilingi ngapi? Na hii ndiyo inajibu hoja mwananchi maskini sera inataka mwananchi kuchangia huduma za afya isipokuwa makundi matatu, lakini kama mtu hana uwezo tumeweka utaratibu wa kuchangia na ndiyo maana nikisoma haraka haraka, Kagera katika kipindi cha mwaka jana wametoa misamaha ya shilingi milioni 170, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa misamaha shilingi milioni 391, Mtwara Ligula misamaha shilingi 67 na Mbeya shilingi milioni 88.

Mheshimiwa Spika, nimesema Dodoma na Kamati imesema kwa hiyo ili suala la msamaha sisi ni jukumu letu kila Mtanzania apate huduma bila ya kikwazo cha fedha, lakini tumeangalia muarobaini wa kwenda nalo mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwelekeo kama ilivyoshauri Kamati ni kuhakikisha tunakuja na bima ya afya kwa kila mtu ili aweze kupata huduma, siyo kwamba tumekaidi ushauri wa Kamati na Bunge, bado tupo katika taratibu na majadiliano ndani ya Serikali lazima tufanye-actuarial study (tathimini ya uhakika) kama kila mwananchi awe na bima je wachangie shilingi ngapi, wapate huduma katika hospitali za binafsi na hospitali za umma. Kwa hiyo siyo jambo la hararaka tumeelekezwa ebu tufanye tathmini ya kina tusije tukaanzisha bima kesho baada ya wiki mbili wananchi wanakosa huduma kwa sababu mfuko umefilisika.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni suala la maendeleo ya jamii, tumepokea ushauri wa Kamati kuhusu kuboresha mitaala/kufanya review ya mitaala ya vyuo vyetu vya maendeleo ya jamii kwamba imepitwa na wakati tunalipokea na tutalifanyia kazi.

Lakini labda ;ingine la kusema amelisema vizuri Mheshimiwa Deo Ngalawa, Mheshimiwa Mbunge the way forward tusiwe pia ni taifa la kulilia tiba tiba, tiba sisi kama Wizara tumeona ipo haya sasa Serikali, jamii na wadau tukawekeza kwenye huduma za kinga, watu wanaumwa kwa sababu hawana vyoo, watu wanaumwa kwa sababu hawazingatii lishe bora, watu wanaumwa kwa sababu hawafanyi mazoezi, hawazingatii ulaji wa vyakula unaofaa wanavuta sigara, wanakunywa pombe kupita kiasi. Kwa hiyo,ili kupunguza mzigo wa fedha wa gharama za kutoa huduma za afya lazima wote kwa pamoja twende katika huduma za kinga badala tu ya kuwekeza katika huduma za kinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni suala la Kamati ya UKIMWI ya Mheshimiwa Mukasa na mimi nimpongeze kwa kweli amekuwa ni msukumo mkubwa sana kwetu sisi Serikali kuhakikisha tunachukua hatua za kuhakikisha tunatokomeza virusi vya UKIMWI na UKIMWI ifikapo mwaka wa 2030 na inawezekana. Kwa hiyo, 90 ya kwanza...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kw amuda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA , WAZEE NA WATOTO: Ya pili au ya kwanza?

NAIBI SPIKA: Ni ya pili Mheshimiwa, lakini malizia dakika moja.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Kwa hiyo, kwenye 90 ya kwanza nataka tu clarify sasa hivi asilimia 77 ya Watanzania wanoishi na virus vya UKIMWI tayari wanafahamu kwamba wanayo maambukizi ya UKIMWI na sasa hivi asilimia 98 ya wanaoishi na virusi vya UKIMWI tumewaingiza katika utaratibu wa dawa na asilimia 88 virusi
tayari vimefubazwa. Kwa hiyo, tunaenda vizuri Waheshimiwa Wabunge sina shaka kwamba tutafika lengo la kutokomeza UKIMWI Tanzania ikifika mwaka 2030 sambamba na kutokomeza kifua kikuu.

Mheshimia Naibu Spika, baada ya kusema hayo nawapongeza Kamati na ninaunga mkono hoja na Wizara tutatelekeza maoni na ushauri wa Kamati pamoja na wajumbe ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
WAZIRI NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nianze Mwenyezi Mungu kwa kunipa kipali cha kusimama tena mbele ya Bunge lako Tukufu, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kuhitimisha hoja yangu kuhusu makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais TAMISEMI, Tume ya Utumishi wa Walimu pamoja na Taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2021/2022. Kwa kutoa ufafanuzi kuhusu michango ya Waheshimiwa Wabunge ambao wametoa katika mjadala wetu wa siku tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge ambao wameweza kupata fursa ya kuchangia hoja yangu, hoja yangu imechangiwa na Waheshimiwa Wabunge 103 ambapo Wabunge 89 wamechangia kwa kuongea na Wabunge 14 wamechangia kwa maandishi, lakini pia Wabunge 46 wamechangia kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee ninawashukuru sana, Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri wenu na katika hatua hii, niseme kwamba tumepokea maoni na ushauri wenu na tutaufanyia kazi. Kipekee nitambue mchango mkubwa wa Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa ambao uliwasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati Mheshimiwa Humphrey Polepole. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli tumepitia mchango wa Kamati umesheheni madini, mazito ya kwenda kuimarisha utendaji kazi wa Mikoa na Tawala za Serikali za Mitaa. Kwa hiyo, tunajibu tu kwa kifupi, lakini naomba niwahakikishie Mheshimiwa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Pamoja na wajumbe wa Kamati yetu yote ambayo mmetushauri tutayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapokea pia pongezi ambazo mmetupatia mimi pamoja na Manaibu Mawaziri, tunawashukuru sana na niseme pongezi hizi hazitatufanya tukapandisha mabega juu, bali litakua ni deni kwetu la kuhakikisha changamoto zilizopo katika mikoa na mamlaka za Serikali za Mitaa, tunakwenda kuzitatua. Tunaweza tusizimalize zote, lakini nataka kuwadhibitishia Waheshimiwa Wabunge, pia kuilinda imani kubwa na heshima kubwa ambayo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amenipa pamoja na Manaibu Mawaziri tutakwenda kufanya kazi na Waheshimiwa Wabunge mtaona matokeo ya kazi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba wizara hii ikifanya vizuri basi tutakua tumeboresha maisha ya watanzania kwa sababu tunagusa maisha ya Watanzania katika ngazi zote, kwenye vitongoji takribani 64,384, vijiji 1,2319, mitaa 4,263, kata 3,956, tarafa 570, halmashauri 184, wilaya 139, pamoja na mikao 26. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na Waheshimiwa Wabunge tunatambua jukumu ambalo tunalo la kuhakikisha kwamba tunaenda kuboresha shughuli za utawala na maendeleo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Hususani katika masuala ya elimu, Afya ya msingi, barabara, pamoja na Utawala Bora ikiwemo usimamizi wa rasilimali fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge zilihusu mambo mengi, lakini makubwa ambayo tumeyabaini ni matano, la kwanza ni miundombinu ya barabara chini ya wakala wa barabara vijijini na mijini TARURA; la pili ni masuala ya afya katika upande wa miundombinu ya kutolea huduma za afya katika zahanati, vituo vya afya, na hospitali zetu, za halmashauri kuna masuala ya watumishi upatikanaji wa dawa vifaa, na vifaa tiba, bima ya afya ya jamii iliyoboreshwa, pamoja na matumizi ya force account katika ujenzi wa miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hoja ya tatu ni elimu ikiwemo pia miundombinu, mazingira bora ya kujifunzia na kufundishia ikiwemo uhaba wa watumishi; eneo la nne ni Utawala Bora na Ukusanyaki na usimamizi wa mapato kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa, lakini kubwa ambalo limejitokeza pia ni posho za Waheshimiwa Madiwani, madeni ya Madiwani kutokana na dhamana na mifumo ya ukusanyaji mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tano ni masuala ya kuwawezesha wananchi kiuchumi hususani wanawake, vijana na watu wenyeulemavu. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge zile hoja binafsi tutazijibu kwa maandishi kuhusu majimbo yenu moja moja. Lakini hapa nitatoa ufafanuzi wa jumla katika masuala haya makubwa matano na nimshukuru sana Waheshimiwa Manaibu Mawaziri kwa kujibu baadhi ya hoja za waheshimiwa Wabunge na Waziri wa Afya kwa kujibu baadhi ya hoja. Kwa hiyo, nitajikita kwenye mambo makubwa mawili Utawala Bora na Usimamizi wa Rasilimali za Umma na pili ni suala la kuwawezesha wananchi kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, labda tu kwa ufupi nitowe msisitizo kuhusu miundombinu ya barabara kama alivyosema Naibu Waziri Dkt. Festo Dugange karibu asilimia 90 ya michango imegusa TARURA. Waheshimiwa Wabunge tumelipokea ili na kama alivyosema Naibu Waziri kwenye hotuba yangu tulisema mtandao wa barabara ambao umepitishwa ni kilometa laki moja na nane, habari njema tunamshukuru Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi wiki hii wameongeza mtandao wa barabara ambao utasimamiwa na TARURA kufikia kilometa 144,427, maana yake dada yangu Anne Kilango Malecela hata lile suala la vigezo vya kugawa, fedha za TARURA linaenda pia kupatiwa ufumbuzi kupitia suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatutaangalia tu ukubwa wa barabara, tutaangalia na masuala ya geografia ya eneo husika, kwasababu tukisema Tanga unipe kwa sababu ninakilometa labda 30 na mama Kilango ana kilometa 10 utupe fedha sawa siyo sahihi kwasababu yeye anamilima na mabonde na kuna mambo mengi ambayo tutazingatia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge naomba niwaahidi tutatenda haki kwa kila jimbo, tutatenda haki kwa kila halmashauri. Lakini jambo la pili ambalo mmeliongea ni kuhusu kuongeza fedha kwa ajili ya TARURA, Serikali imelipokea, Mheshimiwa Waziri Mkuu yuko hapa amewasikia, Waziri wa Fedha amewasikia tutaendelea kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la tatu kuhusu TARURA, Waheshimiwa Wabunge tumesikia maoni na ushauri wenu kwamba hakuna ushiriki mzuri wa Waheshimiwa Madiwani katika kupanga vipaumbele vya Ujenzi, matengenezo pamoja na maboresho ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumelitafakari ili na tumeamua kuanzia mwaka huu wa fedha vipaumbele vyote vya ujenzi, kuboresha na matengenezo ya barabara vitapitishwa na baraza la Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika zile siku tatu za Madiwani kukutana kwa ajili ya kujadili bajeti tunaongeza siku moja kabla itakuwa ni madiwani kujadili vipaumbele vya matengenezo, maboresho, pamoja na ujenzi wa barabara. Kwa hiyo, badala ya kikao cha siku tatu kitakuwa ni kikao cha siku nne na ikiwezekana waende site wakaone hizo barabara ambazo zinapendekezwa kujengwa na kufanyiwa maboresho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwasababu na sisi tunakaa katika Mabaraza ya madiwani, tuzingatie pia ushauri wa wawataalamu wetu tusije tukarudi nyuma kila diwani anataka apewe mita 200 au 300 za barabara. Kwa hiyo, pale ambapo labda tutashindwa kupata consensus, barabara ipi, kwa hiyo, tutaomba baraza la madiwani watuandikie wizara alafu tutafanya maamuzi, lakini tumewasikia, kwakweli ni haki yao madiwani zile ni barabara zao ziko katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwasababu ya muda mradi wa TAKTIK na tumewasikia Wabunge kutoka Manispaa, Majiji na Miji upo kwenye maandalizi na tunaamini kwamba tutaukamilisha kwa wakati. Kwa hiyo, niwatowe hofu Wabunge hususani kutoka majiji, Mheshimiwa Naibu Spika ulisema, Mheshimiwa Mabula Mwanza, lakini na mimi pia Tanga ni mnufaika kwa hiyo kupata kwa Mbeya kutakua kupata kwa Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo tu majiji sita ni majiji, manispaa na miji 45 tumeona manufaa ya mradi huu. Kuhusu DMDP II, watu wa Dar es Salaam tumewasikia na pia tuko katika maandalizi ya mwisho. Kwa hiyo, tunaamini pia kwamba mradi huu tutaukamilisha kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, sasa nijikite katika hoja nyingine mbili; ya kwanza ni suala la utawala na usimamizi wa rasilimali fedha za umma. Tumepokea ushauri wa kamati pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwamba tuzisimamie kikamilifu halmashauri nchini ili kuhakikisha kuongeza makusanyo kwa kuweka malengo halisia. Hili tumelipokea na nikweli halmashauri nyingi zina under bajet hazipangi malengo mahususi ya makusanyo, lakini hata yale makusanyo katika taarifa yangu nimeonyesha hadi mwezi wa pili mwishoni makusanyo ni asilima 58 tu.

Mheshimiwa Spika, na makusanyo hayo kadri tutakavyoyapata ndipo tunaenda kuboresha huduma za jamii katika halmashauri zetu. Kwa hiyo, tumeandaa mwongozo wa usimamizi wa mapato ya ndani revenue administration manual ambayo umeainisha namna bora ya kuandaa mipango na bajeti ukusanyaji na usimamizi wa mapato haya.

Mheshimiwa Spika, pia Ofisi ya TAMISEMI tutaendelea kuwajengea uwezo wataalam wa ngazi za mikoa na halmashauri jinsi ya kuandaa mipango na kufanya makisio ya mapato ya ndani yenye kuakisi uhalisia. Pia sasa hivi ndani ya Wizara tunakamilisha Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (Five Years Revenue Enhancement Strategic) ambapo lengo pia ni kufanya maoteo ya makusanyo kwa kila halmashauri kwa miaka mitano. Kwa hiyo, suala hili tumelipokea na tutaenda kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, suala la pili, Serikali itizame mwenendo wa ukusanyaji na udhibiti wa mapato ya ndani ya halmashauri kwa kutumia machine za kielektroniki (POS). Hili pia tumelipokea na sasa hivi tumeongeza matumizi ya machine za kielektroniki kwa ajili ya kukusanya mapato, tuna takribani machine za POS 26,873. Ndani ya kipindi kifupi tutaongeza machine 2,129 ambazo tutazisambaza katika halmashauri 49.

Mheshimiwa Spika, naomba nikiri tunalo pia tatizo la uadilifu wa baadhi ya watendaji wetu hususani wanaohusika na ukusanyaji wa mapato. Kwa hiyo, hatutasita kuchukua hatua za nidhamu pamoja na kuboresha sheria ndogondogo za halmashauri katika kuhakikisha kwamba mapato yanakusanywa na yanaenda katika njia sahihi na iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha tunaboresha mfumo wa makusanyo unaotumika sasa hivi ili kuondoa kabisa mapokezi ya pesa taslimu kama Waheshimiwa Wabunge mlivyotushauri hapa lakini pia kutowasilishwa benki fedha zinazokusanywa na matumizi ya fedha mbichi kabla ya kuwasilishwa benki. Tunaamini kwamba mfumo huu utawawezesha pia walipa tozo, ushuru na kodi kujua wanachodaiwa, kupata control number na kufanya malipo kwa mtandao kwa wakati na tunategemea utaanza tarehe 01 Julai 2021.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ni kuhusu kuibua vyanzo vipya vya mapato ili kuziwezesha halmashauri kutoa huduma bora. Nalo hili tumelipokea na ndiyo maana pia katika bajeti yetu moja ya kipaumbele tumeeleza pia tunaenda kuongeza nguvu ya kuhakikisha kwamba tunawekeza au tunaziwezesha halmashauri katika kuweka mazingira wezeshi ya kufanya biashara pamoja na uwekezaji. Lengo letu ni kuhakikisha tozo, kero kwa wananchi zinaondoka, tujike kwenye vile vyanzo ambavyo tunajua kwa hakika kwamba vitaweza kutuletea mapato.

Mheshimiwa Spika, taarifa ya CAG imeonyesha kwamba halmashauri zimeshindwa kukusanya takribani shilingi bilioni 31 katika mwaka wa fedha 2020/2021 wakati wenyewe wamesema hiki ni chanzo lakini wameshindwa kukusanya. Kwa hiyo, tumelipokea na hili tutalifanyia kazi ikiwemo pia kuweka miradi ya kimkakati katika halmashauri nyingi kwa sababu pia tumeona ni vyanzo vya mapato.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni katika utawala bora, Kamati na Waheshimiwa Wabunge wameshauri Ofisi ya Rais-TAMISEMI isimamie Sekretarieti za Mikoa kuandaa taarifa za mipago na bajeti za mafungu. Tunakubaliana na ushauri na mimi mwenyewe nataka nikiri nimeona tunalo tatizo. Juzi nilienda kwenye Sekretarieti ya Dodoma, kwa mujibu wa Sheria ya Mamlaka za Serikali za Mitaa imeanzishwa Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa. Huyu Katibu Tawala wa Mkoa ana wataalam wote wa fedha, wahasibu, miundombinu including wahandisi, wanasheria, madaktari na watu wa elimu lakini nikawauliza katika huu mwaka wa fedha wa 2021 mlishakaa na halmashauri yoyote ya Dodoma mkachambua mipango yao ya maendeleo na makusanyo yao; internal auditors mlishawahi kuwaita mkawauliza mnafanya kitu gani hawajawahi kufanya. Kwa hiyo, tunakwenda kuzifumua Sekretarieti za Mikoa, tunakwenda kujenga uwezo wa Sekretarieti za Mikoa kwa sababu sheria inasema wao wana wajibu wa kuzisimamia, kuzishauri na kuzijengea uwezo halmashauri katika masuala mazima ya mapato na maendeleo katika halmashuri zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ofisi ya RAS kuna watu wanaitwa Katibu Tawala Msaidizi wapo kama sita, nane au kumi, wale watu ni wakubwa kuliko Wakurugenzi wa Halmashauri kwa sababu ni Assistant Directors; DED yuko chini ya RAS lakini sasa tumegundua kuna baadhi ya Wakurugenzi hawawaheshimu hawa ambao ni Makatibu Tawala Wasaidizi. Kwa hiyo, pia natuma salama kwa Wakurugenzi wa Halmashauri unapofuatwa na Katibu Tawala Msaidizi kumbuka ni bosi wako unatakiwa kumsikiliza, kumheshimu na kutekeleza maelekezo yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tumeona upande wa pili wa shilingi, kuna baadhi ya hawa Makatibu Tawala Wasaidizi wenyewe hawajiamini na hawana uzoefu. Sasa unaenda vipi kukaa na Mkurugenzi wakati wewe mwenyewe hujiamini na huna uzoefu, ndiyo maana nasema tunaenda kuzifumua Sekretarieti za Mikoa kwa sababu sitegemei Waziri wa TAMISEMI ndiyo azunguke nchi nzima wakati kuna Katibu Tawala wa Mkoa na wataalam zaidi ya tisa katika ofisi yako ambao wana jukumu la kisheria kusimamia halmashauri zetu. Kwa hiyo, hili tunaenda kulifanyia kazi na tutasaini performance contract na Wakuu wa Mikoa kwa sababu wao ndiyo wanasimamia hizi Sekretarieti za Mikoa. Kwa hiyo, ushauri huu tumeupokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la posho za Madiwani kuna hoja mbili; hoja ya kwanza ilikuwa ni kuongeza posho za Madiwani. Tumewasikia Serikali iko hapa itafanyia kazi suala hili. Hoja ya pili ni kwamba posho hizi zilipwe moja kwa moja kupitia ruzuku ya Serikali. Tumelipokea pia na tunakubaliana na maoni ya Waheshimiwa Wabunge kwamba Madiwani wamekuwa wakifanya kazi kubwa na nzuri ya kusimamia shughuli za maendeleo katika majimbo yetu. Mimi nataka kukiri hata mimi nikienda Tanga Mjini namtafuta Diwani yule ndiye mpambanaji wangu, ndiye askari wangu.

Mheshimiwa Spika, tumefanya tathmini ya haraka haraka ya miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2019/2020 halmashauri 97 zimekusanya wastani wa mapato ya ndani chini ya shilingi bilioni mbili, halmashauri 71 zimekusanya wastani wa chini ya shilingi bilioni tano, ni halmashauri 17 tu ndizo zilizokusanya wastani ya mapato ya ndani ya shilingi bilioni tano kwa mwaka. Kwa hiyo, ni kweli kwamba halmashauri nyingi zinashindwa kulipa posho za Madiwani kikamilifu hali ambayo inasababisha kama alivyosema mtani wangu Mheshimiwa Kasalali kwamba Diwani anajiona ni dhaifu mbele ya Mkurugenzi kwa sababu ni Mkurugenzi atakavyoamua na kulipa posho anasema sina mapato. Kwa hiyo, hata ule usimamizi wa halmashauri maana mtu wa kwanza wa kusimamia fedha za Serikali kwenye halmashauri ni Baraza la Madiwani sio mtu mwingine ndiyo inakuja Regional Secretariat. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili naomba niseme tumelipokea na kwa kweli tunakubaliana na nyie kwamba ni sehemu ya kero, bugudha lakini pia kutoheshimisha kada ile ya Madiwani. Serikali imewasikia na tunaendelea kufanya uchambuzi. Tumeangalia tuna Madiwani takribani 5,275 inayojumuisha Madiwani 3,956 wa Kata na Madiwani 1,319 wa Viti Maalum. Niwaombe sana tulibebe hili twende tukafanye uchambuzi zaidi, ikiwemo posho ya Wenyeviti wa Vijiji, Mitaa na Vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa suala la kuboresha mahusiano ya viongozi wa mikoa, wilaya ya halmashauri. Tunalipokea, tutaendelea kutoa elimu na mafunzo kwa viongozi wetu Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, ma-DAS, kuhusu kila mtu kutambua wajibu na mipaka katika kazi zake na majukumu yake na umuhimu wa kufanya kazi kama timu. Niseme tu tumekuwa pia tukishirikiana na Taasisi ya Uongozi kwa ajili ya kutoa mafunzo lakini pale ambapo kumekuwa na mgogoro pia tumekuwa wepesi wa kwenda kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, katika suala la utawala bora, kuna suala la matumizi ya force account, Wabunge wengi mmekubali kwamba ni utaratibu mzuri lakini pia ni kichaka cha upotevu wa fedha. Tunakuliana nanyi, tutaenda kuongeza nguvu ya kusimamia eneo hili lakini tukubaliane kwamba force account imetusaidia sana kwa sababu kuna maeneo Ofisi ya Jengo la Mkuu wa Mkoa tunaletewa bili ya bilioni 1.5 wakati sehemu nyingine inajengwa kwa shilingi milioni 300 au400. Kwa hiyo, tunakubali kwamba ipo haja ya kuimarisha ubora hususani kuwa na Wahandisi na watu wa QS katika halmashauri zetu. Habari njema kwa sababu tuna uhaba wa Wahandisi katika halmashauri zetu, tunao kama 80 katika halmashauri zote 184, tumeongea na Mkuu wa Majeshi ana Wahandisi katika Jeshi, kwa hiyo, tunamuomba ikiwezekana tuwashikize katika halmashauri zetu ili pia waweze kufanya kazi hii ya kutoa ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala la TAMISEMI isimamie na kuhakikisha fedha za uendeshaji katika ngazi za chini za kata na vijiji zinakwenda, hili tutalisimamia. Pia kuna masuala ya halmashauri zinazodaiwa na benki, mikopo ya Waheshimiwa Madiwani iliyotokana na dhamana ya posho za kila mwezi ikamilishwe, hili pia tumelipokea na madeni yameanza kulipwa, hadi Juni 30 madeni ya mikopo ya Madiwani yalikuwa shilingi bilioni 5.5 kati ya shilingi bilioni 10.9 ambazo zimelipwa.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la migogoro na kero za wananchi kwamba tuongeze jitihada za kuhakikisha kwamba tunatatua migogoro ya ardhi, wananchi kunyang’anywa mali zao lakini pia kuna mambo mengine ya mirathi. Nafurahi sana nimeongea na Waziri wa Katiba na Sheria simuoni hapa pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali tumeamua kuchukua hatua ya mpito tunakwenda kuwatumia Wanasheria katika Ofisi za Makatibu Tawala wa Wilaya ambao wapo tutawaongezea jukumu pia la kutoa huduma kwa wananchi katika halmashauri zao ambao wana matatizo ya kisheria hususani migogoro ya ardhi, mirathi pamoja na mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, masuala ya kiutawala yapo mengi Waheshimiwa Wabunge tumeyapokea, lakini kubwa ni kwenda kudhibiti makusanyo ya halmashauri pamoja na matumizi ya Serikali. Ukingalia bajeti hii shilingi trilioni tatu tunazipeleka kwenye halmashauri, maana yake ni lazima tuongeze nguvu ili fedha hizi ziweze kuleta matokeo yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa uwezeshaji wa wananchi kiuchumi, tumepokea maoni au ushauri wa Kamati pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwamba tuongeze umakini katika kusimamia sheria, kanuni na miongozo mbalimbali. Hili wala sihitaji kuchukua muda mrefu, tunakubaliana na ushauri na hususani kwanza kuhakikisha badala ya mikopo ile kuwa inatolewa kiduchukiduchu itolewe kwenye miradi mikubwa ambayo itaweza ku- generate ajira lakini pia itaweza kuleta mapato na faida kwenye halmashauri. Kwa hiyo, tutaweka mgao maana pia tusiwasahau hawa akina mama wangu wanaopika maandazi, wanaochoma mishikaki na vijana hawa wanaouza karanga, kwa hiyo, tunaweza tukasema katika kila hela ile inayotolewa kwa mikopo basi asilimia fulani iende kwa hawa wajasiliamali wadogowadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa kwenye mikopo tumeona ni marejesho kwa mfano katika bajeti hii ambayo tunaenda kuimalisha Juni zilitolewa karibu shilingi bilioni 26 lakini hakuna taarifa ya kiasi gani kimerudi. Kwa hiyo, hapo ndiyo tunaenda kupambana kwa sababu kama bajeti hii tumetenga shilingi bilioni 67 maana yake kwa miaka 5 tuna zaidi ya shilingi bilioni 120 maana yake itakuwa sasa tuna mfuko ambao ni endelevu utaweza kwenda kufanya kazi vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumepokea ushauri kuhusu elimu kwa vikundi hivi pamoja na kuhakikisha tunawatumia vizuri Maafisa Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda nimalize hili la Mheshimiwa Munde Tambwe kuhusu kugawa Mikoa. Ni kweli tuna vigezo kwa ajili ya kugawa mikoa, majimbo, halmshauri na wilaya, niseme tu tumelipokea na tutalifanyia kazi kwa sababu hili pia lina gharama kwa kiasi fulani kwa upande wa Serikali, kwa hiyo, lazima pia tufanye tathmini. Kwa mujibu wa vigezo ambavyo nimeletewa, Mkoa wa Morogoro na Tanga unakidhi vigezo vya kuweza kupata Mkoa mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna hoja nyingine kama nilivyosema za Waheshimiwa Wabunge ambazo ni hoja moja moja tutazifanyia kazi hususani kwenye suala la elimu. Naomba niseme kwamba mimi ni mama na mnaonifahamu mnajua kwamba napenda sana Watoto. Kwa hiyo, katika kazi zangu asilimia kubwa nitasaidiana na Naibu Waziri Silinde kuhakikisha tunaboresha mazingira ya elimu kwa ajili ya watoto wetu. Hakuna urithi wowote wa maana ambao tunaweza kuwapa watoto wetu zaidi ya elimu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwenye hili tutalifanyia kazi kuhakikisha kwamba tunajenga madarasa na tumepokea ushauri wenu; Mheshimiwa Mzanva ndugu yangu Korogwe umesema pia tuangalie hata tunavyofanya mgao wa rasilimali fedha kwamba mwingine ana kata 15 mwingine anakata 35 wote unawapa maboma sawa. Kwa hiyo, hili tumelipokea tutaenda kulifanyia kazi, tutakuwa na minimum na maximum. Kubwa Waheshimiwa Wabunge naomba niseme angalau kila mtu apate, kila Mbunge aweze kwenda kwenye Jimbo lake aseme katika kipindi cha Ubunge wangu nimeleta moja, mbili, tatu, nne, tano. Kwa hiyo, hili tutakwenda kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kukushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kuweza kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge siyo zote lakini zile za mojamoja Waheshimiwa Wabunge tumezipokea na tutaziletea ufumbuzi. Nimshukuru

Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini kusimamia Wizara hii ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Naamini Mwenyezi Mungu ataniongoza vema ili niweze kukidhi matarajio yake na matarajio ya Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais, Dkt Philip Mpango kwa ushauri na kufuatilia kwa karibu masuala ya mapato na matumizi ya halmashauri. Hata kama jana mliniona yale mambo mengine unakuta na Makamu wa Rais naye aliyapata, kwa hiyo, nami nayapata. Kwa hiyo, amekuwa akitupa msaada mkubwa katika kufuatilia masuala ya fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, nakosa maneno mazuri ya kumshukuru. Ukiwa na jambo lolote wakati wowote yuko tayari kukusilikiliza na kutafuta ufumbuzi wa jambo ambalo linakukabili. Mheshimiwa Waziri Mkuu mimi naamini Mawaziri wenzangu wengi tunajifunza kutoka kwako, kutojikweza, kuwa wanyenyekevu, kusikiliza na kutopandisha mabega katika utekelezaji wa majukumu yetu. Mwenyezi Mungu akuzidishie kheri Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekushukuru wewe kwa kuongoza vema Bunge letu na hususani siku mbili umesimamia mjadala wa hoja yangu pamoja na Naibu Spika lakini kipekee kwa mchango mkubwa ambao umeutoa katika kuboresha huduma za elimu katika nchi yetu. Bunge High School itaendelea kuwa alama ya kazi yako kubwa na nzuri ambayo umeifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda sasa ndiyo changamoto tukatafute Bunge Boys School kwenye Bunge la Kumi na Mbili. Mimi nadhani Bunge la Kumi na Mbili tufanye mpango kwa ajili ya Bunge Boys School. Nataka kukuthibitishia na mimi ni mzazi tutahakikisha watoto wote wa kike na wa kiume wanapata haki sawa na huduma sawa za elimu na masuala mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru Naibu Spika kwa kusimamia vyema mjadala katika siku hizi tatu, lakini pia Waheshimiwa Mawaziri wenzangu nawashukuru kama ambavyo ameeleza Mheshimiwa Mbunge wa Kiteto TAMISEMI ni hati ya kila kitu. Kwa hiyo, sisi tunasikiliza miongozo na sera zenu, tuko tayari kutelekeza na tunawathibitishia hata mkituletea rasilimali fedha tutahakikisha zinatumika kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango na ushauri lakini kwa ushirikiano mzuri mnaotupatia. Kipekee niishukuru Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, chini ya Mwenyekiti, Mheshimiwa Humphrey Polepole pamoja na Makamu Mwenyekiti, Mheshimiwa Abdallah Chaurembo kwa ushauri. Kama nilivyosema mafanikio ambayo TAMISEMI inapata ni kutokana na Kamati hii yenye watu wazuri wanaojikita na wako serious katika kuchambua hoja za Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa si lolote kama sitawashukuru wapiga kura wa Tanga Mjini. Nawashukuru sana kwa kunichagua kwa kura nyingi sana kuwa Mbunge wao. Ahadi yangu imekuwa ni kwamba badala ya kuifanya Tanga kuwa Jiji la mahaba na ukarimu linaenda kuwa Jiji la mahaba, ukarimu na maendeleo zaidi, kwa hiyo, ninawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee familia yangu nawashukuru kwa uvumilivu wao hususani napokosa muda wa kuwa nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nakushukuru kwa kunipa fursa hii niweze kuchangia hoja ya Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na wataalam wote kwa kuandaa bajeti nzuri ambayo kwa kweli inakwenda kutatua changamoto katika maeneo yetu katika ngazi za Vitongoji, Vijiji, Kata, Halmashauri na Wilaya. Kwa hiyo, katika hatua hii nasema naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri ambao mmetupatia katika maeneo mbalimbali ikiwemo kuboresha elimu msingi na sekondari, kuboresha huduma za afya ya msingi katika zahanati, vituo vya afya na Hospitali za Halmashauri. Ushauri mzuri mmetupatia kwa ajili ya kuboresha barabara za vijijini na mijini kupitia TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, tumepokea ushauri wenu Waheshimiwa Wabunge kuhusu kuimarisha Utawala Bora ikiwemo usimamizi wa rasilimali fedha katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Waheshimiwa Wabunge, tunawashukuru sana na tunawaahidi kwamba tutafanyia kazi ushauri wenu na tutatoa taarifa kupitia kwenu kupitia Kamati ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijibu mambo makubwa matatu au manne. Jambo la kwanza, Waheshimiwa Wabunge tumepokea ushauri wenu. Kwanza tunapokea pongezi kwa Serikali kupitia Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan ya kuamua kubeba mzigo wa posho za kila mwezi za Madiwani kulipwa na Serikali Kuu. Pia tumepokea maoni yenu kwamba sasa kile ambacho kitaokolewa kiende kikalipe fedha au posho kwa Wenyeviti wa Vitongoji na Vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili linatakiwa kufanya uchambuzi, lakini tumeona mahesabu ya haraka haraka, tunaweza tukapata savings. Mheshimiwa Comrade Mkuchika katika Halmashauri yake ya Mji wa Newala wana Madiwani
22. Kwa hiyo, Madiwani wa Kata ni 16 na wengine ni wa Viti Maalum. Kwa hiyo, kama wangelipa Halmashauri, ni kama shilingi milioni 7.3. Kwa sababu Serikali inabeba huu mzigo; na kwa sababu pia tumeelekeza ile shilingi 100,000 angalau ikalipe posho za watendaji wa Kata, kwa hiyo, ukitoa shilingi milioni 7.3 na shilingi milioni 1.6, Halmashauri itabakiwa au ita-save shilingi milioni 5.7.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, inawezekana kabisa kuwapa hata hela kidogo; shilingi 20,000 ya kuweza kuwasaidia. Kwa hiyo, hili Waheshimiwa Wabunge tumelipokea na tutalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili tumepokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge kuhusu miradi ya kimkakati inayotekelezwa katika Halmashauri zetu hususan masoko yamejengwa au stendi ambayo hayaleti tija au yamekuwa ni kero katika baadhi ya Halmashauri. Tumepata ushauri kutoka kwenye Kamati ya Bajeti inayoongozwa na Comrade Sillo; tumepata ushauri kutoka Kamati ya TAMISEMI inayoongozwa na Comrade Polepole. Kwa hiyo, tutafanya mapitio ya utekelezaji wa miradi yote ya kimkakati. Waheshimiwa Wabunge mtashiriki kuamua miradi hii katika majimbo yenu iende ikatatue kero gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona Watanzania hawataki soko la ghorofa, wanataka simple soko. Kuna roofing, chini kuna floor nzuri, lakini pia ina maeneo mazuri. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, haya tutayashirikisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tatu ni TARURA. Tunawapongeza na kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kueleza kilio chenu kuhusu ubovu wa miundombinu ya barabara katika majimbo yenu na Halmashauri zenu. Ni kweli, TARURA imeanzishwa chini ya Sheria Na. 13 ya 2007 na TARURA inafanya kazi kwa mujibu wa sheria ndani ya Tanzania Bara. Kwa hiyo, mtandao ambao TARURA unahudumia ni kama zenye urefu wa kilometa 100,008.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna utafiti, barabara za lami ni asilimia 2.1, barabara za changarawe ni asilimia 25 na barabara za udongo ni asilimia 72. Kwa hiyo, kwa kweli kilio cha ubovu wa barabara ni kikubwa. Kulikuwa na mvua, kwa hiyo, pia imefanya barabara zetu nyingi hazipitiki na ukiangalia hali ya barabara ni asilimia 23 tu ya barabara zetu kwa mujibu wa Taarifa ambazo ninazo ndiyo ziko katika hali nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tumesikia kilio cha Waheshimiwa Wabunge. Namshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan na Waziri wa Fedha, kwamba sambamba na fedha ambayo tunaipata kupitia Mfuko wa Barabara Mheshimiwa Waziri Chamuriho ameeleza, kuna fedha angalau Hazina walitutengea kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya barabara. Ndiyo maana katika ile dhamira ya Mheshimiwa Rais Samia ya kuwashirikisha Wabunge, tukasema badala ya kuwaachia wataalam waamue fedha hizi ziende wapi, tukaona kila Mbunge tutende haki na usawa kwa kila jimbo, shilingi milioni 500. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nieleze, ninaposema kila jimbo, ni jimbo ndani ya Tanzania Bara kwa sababu TARURA kwa mujibu wa sheria inafanya kazi ndani ya Tanzania Bara. Kwa hiyo, naomba niweke vizuri hili. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge shilingi milioni 500 siyo nyingi lakini tunaamini inaweza kuleta mabadiliko makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kesho Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ana mambo mazuri zaidi anakuja nayo. Mapendekezo yetu Waheshimiwa Wabunge, kwenye nyongeza hii ambayo tutapata kutoka Hazina, Wabunge wa Dar es Salaam mnisamehe, mtapata DMDP II. Kwa hiyo, hatutawaingiza kwenye fedha itakayoongeza, kwenye hela ya Mheshimiwa Dkt. Mwigulu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kuna miji 45 tunategemea itapata fedha kupitia mradi wa TACTICs. Kwa hiyo, tutawoandoa pia kwenye fedha hizi ambao Mheshimiwa Dkt. Mwigulu atatupa. Kwa hiyo, Wabunge tunaamini badala ya shilingi milioni 500 mnaweza mkajikuta mnaondoka hata na 2B. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa namsafishia njia Mheshimiwa Dkt. Mwigulu. Kwa hiyo, mambo mazuri tutayasikia kesho. Wabunge wa Dar es Salaam DMDP II, mambo mazuri; Wabunge wa Majiji 45, Mheshimiwa Naibu Spika, nawe ni mnufaika. Mambo pia yanakuja vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la nne ni la kuboresha miundombinu ya elimu msingi na sekondari. Waheshimiwa Wabunge tumepokea ushauri wenu lakini kubwa zile shilingi milioni 600 tunawaomba sana, tunataka shule iliyokamilika, yenye madarasa nane, yenye vyumba vya maabara vitatu. Yenye nyumba mbili za walimu; two in one na yenye vyoo. Kwa hiyo, mnaposema tuwagawie kidogo kidogo, Waheshimiwa Wabunge tunaomba sana, hebu tufanye kitu complete kipendeze katika majimbo yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuwapa siri nyingine, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu kesho anakuja na mambo mazuri zaidi. Tutatoa fedha za kujenga madarasa haya mawili mawili, manne manne katika shule zenu zaidi ya 10 au nne katika majimbo yenu. Kwa hiyo, haya tunawaomba sana, shilingi milioni 600 hii ikatumike kufanya kazi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dada yangu Mheshimiwa Prof. Ndalichako tunafanya kazi nzuri na Mheshimiwa Dkt. Mwigulu. Tuna network, tuachieni, tutawatafutia fedha chini ya Rais Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kujenga miundombinu ya elimu, miundombinu ya afya na pia miundombinu ya afya katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona hili nilitolee ufafanuzi. Kwa hiyo, tunaomba shilingi milioni 600 ile msiende kuikata kidogo kidogo. Nami nimeshawaambia watu wangu, kama tunampa Mbunge kwenda kuongeza madarasa, lisiwe chini ya madarasa mawili. Kwa hiyo, kila Mbunge kama atapata, angalau madarasa mawili, matatu au manne kwa ajili ya shule za msingi na sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo ningependa kulisisitiza samahani sana Waheshimiwa Wabunge; sambamba na fedha ambazo tutazitoa kutoka Serikali Kuu nataka nikiri katika miezi miwili ambayo nimekuwa Waziri wa TAMISEMI, kuna ubadhirifu au matumizi mabaya ya fedha za Serikali katika Halmashauri zetu. Fedha zinapigwa ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge. Baadhi ya Halmashauri hawajali. Tukiwabana Halmashauri; nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge, nasi sote ni Wajumbe wa Kamati za Fedha; wewe uliza, nataka kuona asilimia yangu 40 ambayo itaenda kutatua kero za ndugu yangu pale Jimbo la Tandahimba, kaka yangu. Kwa hiyo, mnatakiwa mkikaa, usikubali tu wakiwaambia ukarabati, sijui kumalizia, ndiyo wanapiga fedha. Mwulize umekarabati kitu gani? Umekarabati msingi? Umepiga rangi? Umeweka bati? Umeweka dari? Au umeweka floor chini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuwaambia Waheshimiwa Wabunge bila kupepesa macho, tunazo fedha siyo nyingi, lakini zinaweza kwenda kutatua kero za wananchi wetu katika elimu na afya. Pia kuna Halmashauri zinapata zaidi ya shilingi bilioni 500. Waheshimiwa Wabunge, siyo vibaya kuweka bilioni moja kwenda kupiga kilometa mbili za lami katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kaka yangu Mheshimiwa Tarimba nadhani anafahamu, Kinondoni wanapata shilingi bilioni 33, wanatakiwa kupeleka kwenye maendeleo shilingi bilioni 19 kwa mwaka mmoja. Mheshimiwa Gwajima, ninyi sio masikini, yaani mna uwezo wa kupiga sekondari mbili za ghorofa kila mwaka za shilingi bilioni mbili mbili. Mna uwezo wa kupiga vituo vya afya viwili vya ghorofa kila mwaka, shilingi bilioni mbili mbili; kwa Mheshimiwa Gwajima na Kinondoni. Nawaomba sana tushiriki kuwasimamia Halmashauri zetu. Nasi tutajitahidi kuwapitia Waweka Hazina wa Halmashauri wote. Mama akishamaliza kuteua Wakurugenzi, tunaenda kufanya mapitio ya Waweka Hazina wote, lakini pia tunaenda kufanya mapitio ya Maafisa Mipango wote. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia kengele ya pili. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na Mwenyezi Mungu awabariki. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza na mimi niseme naunga mkono hoja. Lakini pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kusimamia vyema raslimali zetu za nchi.

Mheshimiwa Spika, kadiri tunavyosimamia fedha za nchi maana yake tunawekeza pia katika kuboresha huduma za jamii ikiwemo huduma za afya. Nitoe mfano bajeti ya dawa ya Serikali mwaka 2015 ilikuwa shilingi bilioni 24 mwaka 2016 shilingi bilioni 251, mwaka 2017 tunazungumzia takribani shilingi bilioni 269; kwa hiyo kuna watu wanatakiwa waangalie uhusiano wa hatua ambazo tunachukua katika kusimamia raslimali za nchi, lakini pia katika kuboresha huduma za jamii ikiwemo huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupitia jitihada za Mheshimiwa Rais tumeona kwamba kwa mara ya kwanza hakuna Mtanzania mgonjwa atakuwa analala chini kwa sababu tu ya ukosefu wa vitanda au magodoro. Endapo mgonjwa atalala chini ni kwa sababu hospitali au kituo hicho hakina sehemu ya kuweka vitanda au magodoro, hizi zote ni juhudi za Mheshimiwa Rais, Dkt.John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Spika, tumeona kwa mara ya kwanza Mheshimiwa Rais akisambaza vifaa katika halmashauri zote nchini haijawahi kutokea katika historia ya Tanzania. Tumeona kwa mara ya kwanza ambulance zaidi ya 67 Mheshimiwa Rais akizisambaza nchi nzima, haijawahi kutokea katika historia ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba sasa pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kaka yangu Dkt. Mpango na Naibu Waziri, wifi yangu Dkt. Ashatu Kijaji na wataalamu wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri waliyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sekta ya Afya tutanufaika sana na bajeti hii ambayo inapendekezwa. Kwa mfano Suala la kuendelea kutoza ushuru wa forodha wa asilimia 10 katika sukari ya viwandani maana yake ni kwamba tunawekeza katika utengenezaji wa dawa, viwanda vya dawa vinatumia pia sukari ya viwandani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mpango tunakupongeza sana kwa sababu asilimia 80 ya mahitaji yetu ya dawa tunayanunua kutoka nje ya nchi. Kwa hiyo, sasa hivi tunataka kuhakikisha kwamba dawa zinatengenezwa ndani ya Tanzania, hii ni hatua nzuri na tunaipongeza sana.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tunapongeza bajeti hii kwa sababu imefuta ada ya kuanzisha maduka ya dawa. Tumesema MSD haiwezi kuwa na dawa aina zote kwa asilimia 100; kwa hiyo, lazima yawepo maduka binafsi ya dawa. Mheshimiwa Mpango tunakupongeza kwamba umefuta ada ya kuanzisha maduka ya dawa maana yake dawa zitapatikana katika vijiji, katika mitaa yetu na katika makazi yetu. Dawa si biashara, dawa ni huduma tunawapongeza sana Wizara ya Fedha kwa kuliona suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ambalo tunaona sekta ya afya tutanufaika sana na bajeti hii ni suala la kuwatambua rasmi wafanyabiashara wadogo wadogo wamachinga, mama ntilie, maana yake tutakapowatambua ndiyo pia itakuwa rahisi kwetu kuwafikia katika huduma za social security (huduma ya hifadhi ya jamii) na hapa nazungumzia bima ya afya. Endapo wafanyabiashara hawa wadogo tutaweza kuwatambua maana yake pia itakuwa rahisi kwetu sisi kuwafikia na kuwahimiza wajiunge na bima ya afya.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa ya kupata huduma za afya kwa Watanzania ni suala la gharama ya fedha, kwa hiyo tunahimza wananchi wote wajiunge katika mifuko ya bima ya afya ili sasa iwe rahisi kupata dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho ambalo nilitaka kupongeza bajeti hii ni suala pia la kufuta tozo katika mabango ambayo yanaonesha zahanati, sehemu za huduma, vituo vya afya na hospitali, hili ni jambo zuri kwa sababu litakuwa pia ni rahisi kwa wananchi hasa kwa wakati wa dharura kuhakikisha kwamba wanapata huduma za afya kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizi sasa nijikite katika kujibu hoja tatu ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Hoja ya kwanza imeongelewa na Mheshimiwa Lucy Mayenga, naye alikuwa anazungumzia kuhusu utendaji kazi wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, na kwamba kuna kampuni inaitwa Techno Net Scientific Limited ambayo inaingiza kemikali bila kufuata sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru sana Mheshimiwa Lucy Mayenga, tunakubaliana kwamba ndiyo changamoto hii ipo lakini tumeibaini na sasa hivi tayari Mkemia Mkuu wa Serikali anashirikiana na vyombo vingine vya dola kuhakikisha kwamba tunampeleka mahakamani haraka iwezekanavyo Kampuni hii ya Techno Net Scientific ambayo inajihusisha na shughuli za kuhifadhi na kuuza kemikali za viwandani na majumbani wakati usajili wake umeisha toka tarehe 30 Aprili, 2016. Kwa hiyo, Mheshimiwa nikuthibitishie kwamba uchunguzi umekamilika na ndani ya muda mchache tutampeleka mahakamani mhusika.

Mheshimiwa Spika, nitumie Bunge hili kutoa onyo kwa wote wanaojihusisha na kuingiza kemikali za viwandani na majumbani kuhakikisha kwamba wanazingatia sheria.

Mheshimiwa Spika, mwezi wa tisa tulikuja Bungeni tukaleta sheria ya kuibadilisha Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali iwe Mamlaka (Authorty) maana yake ni kutaka kuipa nguvu na uwezo wa kuweza kusimamia shughuli zake mbalimbali ikiwemo kusimamia kemikali za viwandani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Lucy Mayenga nikusihi dada yangu kwamba ndugu yangu tusiifute hii ofisi kwa sababu licha ya kusimamia shughuli za kemikali, lakini pia ina majukumu mengine ya kuhakikisha inasimamia Sheria ya Teknolojia ya Vinasaba, lakini pia inajihusisha na sheria zinazohusika na vilelezo za sampuli katika makosa ya jinai na Mheshimiwa Mwingulu anaitegemea sana katika kukamilisha mashauri mbalimbali ya kijinai ikiwemo Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo limeelezwa na Mheshimiwa Mbunge Aeshi Hilaly ni suala la uvutaji shisha, kwamba je shisha ina madhara gani? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa fursa hii hili niweze kuhitimisha hoja yangu na nianze kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri wenu ambao mmetupatia ili tuweze kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa watanzania. Kipekee tushukuru sana maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii chini ya mwenyekiti wetu Mheshimiwa Stanslaus Nyongo kwa kweli wanatupa ushirikiano mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba maoni na ushauri wa Wabunge tumeuchukuwa na tutaufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee kwa kweli niwashukuru niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa pongezi ambazo mmetupatia, mmetutia moyo mmetupa ari mmetupa nguvu ya kuendelea kusimamia Sekta ya Afya nchini na ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri tuna deni kubwa sana kwenu Waheshimiwa Wabunge tuna deni kubwa sana kwa watanzania na tuna deni kubwa sana kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, tunatambua dhamana kubwa tuliyonayo katika wizara hii, afya ni jambo kubwa afya ni jambo linalomgusa kila mtanzania awe tajiri awe maskini. Kwa hiyo, tunawaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba tutasimamia vyema Sekta ya Afya nchini kuhakikisha watanzania wanapata huduma za afya afya ni mali afya ni mtaji afya ni uchumi.

Mheshimiwa Spika, kipekee nishukuru Wabunge ambao wamechangia tumepata wachangiaji 31 nikiongeza Mheshimiwa Naibu Waziri na Mwenyekiti wa Kamati lakini pia kuna Wabunge kumi wamechangia kwa maandishi na Wabunge saba walichangia wizara yangu wakati wa mjadala wa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, tuseme kwamba yote ambayo Wabunge wamechangia tutayafanyia kazi na kubwa tumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa maono yake, kwa utashi wake, kwa dhamira yake ya kutaka kuona watanzania wanapata huduma bora za afya, hususan afya ya uzazi mama na mtoto. Kama mtakumbuka Wabunge ambao mlikuwa katika Bunge la kumi na moja, Rais Samia Suluhu Hassan akiwa Makamu wa Rais alijifanyisha kazi usiku na mchana ni kama vile alikuwa ndiye namsaidia kuhusu Sekta hii ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alikuwa anafuatilia huduma za Afya alianzisha kampeni ya jiongeze tuwavushe salama ili tuweze kuokoa wanawake wajawazito Rais Samia huyu ndiye aliweza kuzindua chanjo ya kuwakinga wasichana dhidi ya saratani ya mlango wa kizazi, ndio alitusukuma tukapata fedha kutoka Benki ya Dunia kwa mara ya kwanza kujenga Vituo vya Afya vitakavyofanya upasuaji wa dharula ikiwemo kumtoa mtoto tumboni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hayo yalikuwa pia ni maono ya Rais Samia Suluhu Hassan alituwezesha kuzindua pia kampeni ya usichukulie poa nyumba ni choo ambapo pia tunaona sasa kaya za watanzania zina vyoo. Kwa hiyo, suala la afya kwetu sisi tunafahamu kwamba linamgusa kwa karibu sana Rais wetu Samia Suluhu Hassan. Pia ameingia madarakani tumeona fedha nyingi zinaenda kwenye miundombinu kwenye ambulance kwenye watumishi.

Mheshimiwa Spika, kipee pia nimshukuru Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.Mheshimiwa Waziri Mkuu kwetu sisi ni mlezi, mwongozaji, ni mwongoza njia amekuwa akituelekeza usiku na mchana kufanyia kazi changamoto mbalimbali za Sekta ya Afya, Mheshimiwa Waziri Mkuu tunakushuru sana kwa usimamizi wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge ni nyingi lakini naomba niongee kwa sababu ya muda hoja kama tano au sita ya kwanza ambayo imeongelewa na Waheshimiwa Wabunge wengi ni suala la upatikanaji wa dawa na vifaatiba katika vituo vyetu vya kutoa huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ufupi ni kwamba hoja hii sisi tutaenda kuifanyia kazi zaidi tumegawanya katika maeneo makubwa matatu eneo la kwanza ni ngazi ya wizara, tutahakikisha tunakata maoteo sahihi ya mahitaji ya dawa na vifaatiba. Kama Jiji langu la Tanga linasema litatumia kwa mwaka kopo za paracetamol 100 kwa hiyo, lazima tutaangalia je wamepata kopo 100 katika kipindi hiki na hii ndio hoja ambayo pia imeangaliwa imesemwa na Waheshimiwa Wabunge kutumia TEHAMA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, TEHEMA itatusaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha huduma za afya lakini pia sambamba na maoteo tutasimamia miongozo ya kamati za dawa therapeutic committee mwongozo wa standard treatment guideline wa matibabu ya kitaifa na miongozo mingine. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Kingu kwa kuleta hoja ya kuanzisha drug revolving fund kwa kweli hili jambo litasaidia uwepo wa upatikanaji wa dawa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tutafanya audit ngazi ya pili ni bohari ya dawa MSD kwanza nimeshawaelekeza MSD tutawapima kwa upatikanaji wa dawa za miezi minne na sio mwezi mmoja hili tumewaambia tunataka dawa zote 290 pamoja na vifaatiba vipatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili pia tunamshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan kwa maagizo yake tumeshaanza kuyafanyia kazi sambamba na Mheshimiwa Rais kubadilisha uongozi Mtendaji Mkuu wa MSD pamoja na kumteuwa Mwenyekiti wa Bodi tunawaondoa Wakurugenzi watano wa MSD. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkurugenzi wa Fedha MSD anaondoka, Mkurugenzi wa Manunuzi MSD anaondoka, Mkurugenzi wa Logistic wa MSD anaondoka, Mkurugenzi wa Sheria wa MSD anaondoka, na Mkurugenzi wa Utawala wa MSD wanaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tumeshauriwa pia tutaenda kuwaangalia na mifumo supply chain system mifumo ya usambazaji wa dawa ndani ya MSD lakini kubwa tutaendelea kuitaka MSD kununua dawa na vifaatiba kutoka viwandani, kwa kuzingatia mikataba ya muda mrefu. Lakini Waheshimiwa Wabunge naomba niseme jambo moja nimepewa dhamana ya kusimamia sekta ya afya hatuta- compromise ubora wa dawa na vifaatiba kwa sababu tusije tukaenda kuwapa matatizo watanzania kwa kutoangalia ubora wa dawa na vifaatiba kwa hiyo, jambo hili tutalisimamia kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nimpe pole Mkurugenzi mpya wa MSD umepewa hongera lakini jana nilimwambia una kazi kubwa sana kwa sababu matumaini ya Mheshimiwa Rais ya Wabunge na mimi mwenyewe kwake ni makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusema Tukai Mavele alikuwa ndiye mshauri wa Serikali kuhusu masuala mazima ya dawa akiwa upande wa ubalozi wa Marekani Mwenyekiti wa Bodi Rosemary William Slaa alikuwa ndio mshauri wa Serikali kwa upande wa Global Fund ambao wanatupa dawa za UKIMWI TB na Malaria. Kwa hiyo, juzi nilikuwa namwambia Mheshimiwa Waziri Mkuu ni sawa Rais amewaambia nyie si mnatukosoa nyie si mnashauri haya sasa nendeni mkafanya hayo ambayo mlikuwa mnayaeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo DG MSD una kazi kubwa na Waheshimiwa Wabunge nataka kusema tumemwambia tunataka ndani ya miezi mitatu dawa zifike katika vituo na hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho katika eneo hili la dawa ni suala la matumizi ya dawa katika ngazi ya hospitali na vituo, MSD anaweza akapeleka dawa lakini je madaktari wetu na wataalam wetu wanazingatia miongozo ya matibabu ya Kitaifa? Kwa sababu ziko taarifa tumezipata dawa ambazo zipo katika hospitali zilizonunuliwa na Mfamasia zilizoagizwa na Mfamasia daktari anaandika dawa zake mwenyewe ambazo ni kinyume na standard treatment guideline kwa hiyo hili tutalisimamia kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia Waheshimiwa Wabunge mtusaidie mnapokaa kwenye mabaraza ya Madiwani ni lazima tuhoji kamati za afya za kusimamia vituo je zinafanya kazi je zinafuatilia upatikanaji wa dawa. Lakini kubwa kwenye eneo la dawa ni TEHAMA mifumo ya TEHAMA itatusaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha mnyororo mzima wa dawa. Lakini kamati pia imetoa maoni kuhusu matumizi holela ya dawa tutaendelea kuyafanyia kazi eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo pia la mwisho katika dawa tutafufua au kuimarisha uzalishaji wa ndani wa dawa kiwanda cha Keko tutapata fedha tuweze kuwekeza kununua mashine za kisasa na kiwanda kile cha TPI Arusha ambacho pia kimeelezwa na Mheshimiwa Catherine Magige tutahakikisha pia tunapata wawekezaji tayari kesi imemalizika mahakamani TR anafanya mawasiliano tunatafuta wawekezaji waweze kufufua kiwanda kile cha TPI ambacho kipo Arusha pamoja na kuendeleza viwanda vingine vya Keko na Idodi.

Mheshimiwa Spika, suala la Bima ya Afya hili niseme tutaendelea kutoa elimu kuwahamasisha watanzania kuona umuhimu wa kuwa na Bima ya Afya ili waweze kupata huduma za matibabu kabla ya kuugua. Lakini pia tutakamilisha haraka Muswada ule wa sheria wa Universal Health Insurance.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa huduma za kinga Mheshimiwa Shigongo amesema jambo zuri pamoja na Dkt. Paulina pamoja na Mheshimiwa Cecilia Paresso ni kweli ukiangalia hii bajeti tunazungumzia tu tiba tunatakiwa pia ku- foccus kwenye preventive Intervention.

Mheshimiwa Spika, na mimi ndio maana ukiniuliza waziri chagua kipaumbele chako cha kwanza sina hela nitafanya chanjo za watoto kwa sababu ile ni moja ya njia ya kuwakinga Watoto. Lakini Mheshimiwa Shigongo kuhusu homa ini tunakubaliana na wewe kwamba nalo ni janga kwa sababu prevalence ni asilimia 4 kwa hiyo tayari nimeshamwelekeza Katibu Mkuu ule mpango wa Taifa wa kupambana na UKIMWI tunaenda kuubadilisha utakuwa ni Mpango wa Taifa wa kupambana na UKIMWI pamoja na homa ya ini. Kwa hiyo, tunakuwa na integrated programme tutaamasisha wananchi wapime na wapate chanjo ikiwemo kuhakikisha wanapata chanjo kwa gharama nafuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Furaha Matondo umezungumza saratani ya mlango wa kizazi kwa uchungu mkubwa. Ni kweli ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge katika mikutano yetu saratani zinazoongoza kuwakumba watanzania ni saratani ya matiti na saratani ya mlango wa kizazi kwa hiyo, naomba pia tuendelee kuwaambia wazazi na walezi wawapeleke watoto wetu hasa wa kike kupata chanjo ya kuwakinga na maambukizi ya saratani ya mlango wa kizazi.

Mheshimiwa Spika, suala la kinga pia Mheshimiwa Dkt. Paulina tutaweka nguvu katika environmental health katika usafi na afya ya mazingira hivi kwa nini vijiji vyetu na miji yetu ni michafu, kwa nini kuna mabwana kwa nini hatufyeki nyasi kwa nini hatuwekezi katika kuhakikisha pia tunazingatia kanuni za usafi na afya bora kwa hiyo, ni eneo ambalo tutalipa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, lakini pia suala la kinga amezungumza Muuguzi mzuri Mheshimiwa Tecla NCD (non- communicable disease) ni jambo ambalo linaongezeka kila siku na hela hii ya bajeti Waheshimiwa Wabunge haitatosha hata siku moja kama hatutadhibiti magonjwa yasiyoyambukiza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sambamba na kutoa elimu ya watu kuzingatia ulajji wa vyakula kuwekeza kwenye kupima kuepuka unywaji wa pombe kupita kiasi kuvuta sigara lakini pia tunataka kuhakikisha kwenye zahanati wananchi wanapata huduma za kupima au kufanya uchunguzi ili tuweze kugundua mapema magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ukisubiri saratani imefika hatua ya nne hatua ya tatu inakuwa ni matibabu yanakuwa kidogo ni ghali lakini pia hatupati matokeo mazuri. Suala la afya ya uzazi mama na mtoto mdogo wangu Mheshimiwa Husna ameongea kwa uchungu lakini pia mtani wangu Mheshimiwa Kabula pamoja na Mheshimiwa Mabula. Kwanza nataka kusema hatujabadilisha sera ya afya sera ya afya inasema huduma kwa akina mama wajawazito na watoto wa chini ya umri wa miaka mitano ni bure.

Mheshimiwa Spika, nimefundishwa kusema ukweli hiyo sera inatamkwa ni bure kihalisia ni kweli wanawake wengi hawapati huduma za bure kwa ajili ya akinamama na Watoto. Kwa hiyo, hili tunalichukuwa tunafanya calculations kwa mfano mwanamke anapoenda clinic anapoenda kuhudhuria uzurio la kwanza na la pili na tatu na la nne anatakiwa kuangalia wingi wa damu anatakiwa kupimwa urine ili tuangalie kama kuna maambukizi yeyote katika mkojo ili kuhepusha kifafa cha mimba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia shinikizo la damu afanyiwe pia na ultra sound kwa hiyo, tunafanya calculation tuone ni gharama zipi ambazo tunaweza kuzibeba kama Serikali na wananchi tuone ni gharama zipi lakini Bima ya Afya tunaamini ndio itakuwa ndio mwarobaini wa sera hii ya bure au ya msamaha kwa wagonjwa wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili kwa upande wa mama na mtoto ni suala la ubora wa huduma tunakubaliana nanyi Waheshimiwa Wabunge amesema pia Mheshimiwa Paresso kama asilimia 99 ya wanawake wanaenda clinic je wanapata huduma bora na Waheshimiwa Wabunge mimi sina ajenda nyingine nilivyorudi Wizara ya Afya ajenda yangu ni ubora wa huduma na sio bora huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunataka Watanzania wapate huduma bora za afya akifika pale achunguzwe vizuri apate vipimo vyote apate dawa anazohitajika mmesema vizuri Waheshimiwa Wabunge hata ile lugha tu mgonjwa pale tayari ni mgonjwa, anapoenda pale anafokewa ananyanyaswa anasemwa tayari unamwongezea magonjwa kwa hiyo, hili ni eneo ambalo tutalipa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, kwenye hii huduma za afya mama na mtoto Waheshimiwa Wabunge kama alivyosema Naibu Waziri tunawabana wizarani tuna fedha nyingi nataka kukiri sisi Wizara ya Afya tuna fedha nyingi za wadau lakini hatuoni matokeo ya fedha hizo ambazo hizi zinawekezwa tumefumuafumua tumepata NICU (Neonatal Intensive Care Unit) vyumba vya watato wachanga mahututi 100 tunaenda kujenga katika Hospitali za Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumepata fedha kwa upande wa Benjamin Mkapa tunakwenda kuanza kujenga Hospitali ya Taifa ya mama na mtoto lakini pia tutajenga hospitali ya saratani, kwa hiyo hili ni eneo ambalo tutalipa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la afya ya akili Mheshimiwa Jesca Msambatavangu ameongea hapa kama kiutani lakini ni jambo kubwa sana na mimi nimeshawa-challenge watu wangu ni lazima pia tutoe taarifa na kuwekeza katika afya ya akili na bahati mbaya Tanzania afya ya akili tunaichukulia kama criminal issue kama suala la jinai hapana ni suala la afya na hapa tunaweza tukajiona wote tuko sawa lakini afya ya akili ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Jesca kama utaridhia naomba nimteuwe Mheshimiwa Jesca Msambatavangu kuwa balozi wa Afya ya Akili nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu hili jambo lazima tusione aibu kulisema hata nyumbani ndoa divorce frustration ni kwa sababu pia ya afya ya akili, hata huu ukatili nilikuwa naongea na Waziri Gwajima wiki iliyopita hivi baba mzazi unambaka vipi mtoto wako wa miaka minne, mitano kama sio tatizo la Afya ya Akili tumeongea kwa kweli hili jambo tutalipa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la afya kwa watu wenye ulemavu Mheshimiwa Hadija Taya umeliongea vizuri na hili bahati nzuri nimeshaongea na wataalam wangu nimewaambia taarifa zetu za Wizara ya Afya nataka pia tulipoti kuhusu rehabilitative services huduma za utengamao ikiwemo huduma kwa watu wenye ulemavu. Mheshimiwa Stella Ikupa amekuwa akizungumza huduma za wanawake wenye ulemavu katika kujifungua kwa hiyo tumeshapeleka maombi tunaifumua Wizara ya Afya pia nimesema lazima tuwe na kitengo maalum unit ambayo itahusika na masuala ya rehabilitative services huduma za utengamao ikiwemo huduma kwa watu wenye ulemavu na watoto wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, nimepigiwa kengele ya kwanza niseme tu kuna suala la gharama za kuwaona daktari ni kubwa ni kweli na hata jana nawa-challenge watu wangu tumegeuza hospitali kama vile TRA, hospitali kazi yetu ni kutoa huduma sio kukusanya mapato kwa hiyo, sasa hivi unakuta gharama kubwa na nimemuomba Waziri Mkuu ridhaa ukiangalia mwongozo ule ni wa 1997 nitatoa mwongozo wa kusema zahanati ya kumuona daktari isizidi kiasi gani, Kituo cha Afya isizidi kiasi gani, Hospitali ya Wilaya isizidi kiasi gani Hospitali ya Rufaa ya Mkoa isizidi kiasi gani na Hospitali za Taifa isizidi kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunawaumiza watanzania na ndio maana wanakimbilia kwenda kuwaona waganga wa kienyeji, Mheshimiwa Tabasam pia nimpokea mchango wako wa maandishi gharama za dialysis ni very expensive mtanzania gani ataweza kulipa laki mbili na nusu kwa siku mara tatu ni laki saba na nusu kwa wiki, kwa hiyo, ni eneo hili nalo Rais Samia ameshatuelekeza tunalifanyia kazi na tutahakikisha huduma bora za wagonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunarudi kulekule kabla hujaenda kuhitaji dialysis tunataka tuepuke tujikinge na magonjwa haya yasiyoyakuambukiza watanzania nawaomba sana tuwekeze kwenye afya zetu kwa kujali tunavyokula tujiulize wangapi mmekula mboga, wangapi mmekuala matunda katika wiki hii tumeambiwa angalau bia usinywe nyingi bia mbili tatu kwa siku lakini watu wanapiga mpaka bia 10/15 sigara kupita kiasi, pombe.

Mheshimiwa Spika, muda hautoshi. Nimalize kwa kukushukuru wewe kwa kusimamia vizuri mjadala huu. Narudia tena kwa Waheshimiwa Wabunge, afya siyo jambo la kuchekea chekea, afya ni jambo kubwa. Tunatambua dhamana kubwa ambayo tumepewa ya kusimamia afya za Watanzania.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, amekuwa mwepesi sana wa kufanya ziara katika majimbo, lakini amekuwa mwepesi sana wa kusimamia masuala ninayoyaelekeza. Mheshimiwa Dkt. Mollel nakushukuru sana. Nimshukuru Katibu Mkuu Prof. Makubi pamoja na Naibu Katibu Mkuu, Shekalaghe pamoja na Mganga Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema; samahani mtani wangu Mheshimiwa Kabula na Mheshimiwa Mkundi wa Ukerewe, hii tunavyofumua, fedha ziko Wizara ya Afya. Nataka kuwaambia, fedha zipo. Tunakwenda kununua ambulance boat mbili kwa ajili ya Ukerewe na Mafia ili tuwezeshe pia rufaa za wagonjwa katika maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, nimeshamwelekeza Katibu wangu Mkuu kuwasiliana na Katibu Mkuu TAMISEMI tufanye assessment ya zahanati zote nchini, wana vipimo gani na vipi hawana? Vituo vya afya na hospitali, tutakwenda kununua kwa kutumia fedha hizi ambazo zipo, zinatumika kwa ajili ya semina, kwa ajili ya safari, kwa ajili ya kongamano, kwa ajili ya mambo ambayo hayawagusi wananchi moja kwa moja. Jana nimewauliza wenzangu Wizarani, mnaposema tumefanya hivi, mimi Waziri na Naibu Waziri tutasimama kwenye mkutano wa hadhara kuwaambia Watanzania, tumetumia Shilingi bilioni 10 kwa ajili ya semina, kwa ajili ya kongamano, kwa ajili ya matamasha, Hapana. Fedha tutaipeleka kwenye mambo yanayowagusa Watanzania hususan wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalize kwa kukushukuru, pia kuishukuru sana familia yangu, kuwashukuru wapiga kura wangu wa Jiji la Tanga. Tanga tunasema, jiji la mahaba na ukarimu, lakini tunataka liwe la mahaba, ukarimu na maendeleo zaidi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutufikisha siku ya leo lakini kipekee nimshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya afya. Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wote ni mashahidi Bajeti ya Wizara ya Afya mwaka jana Fungu 52 ilikuwa shilingi trilioni 1.1 mwaka huu tunaomba mtupitishie shilingi trilioni 1.2 kuna ongezeko la shilingi bilioni 100.

Mheshimiwa Spika, bajeti ya Sekta ya Afya, ukiangalia fedha zilizotengwa kwenye Wizara ya Afya na fedha za TAMISEMI, bajeti ya Sekta ya Afya imeongezeka kutoka shilingi trilioni 2.1 mwaka jana hadi shilingi trilioni 2.4. Hii inaonyesha dhamira ya dhati kabisa ya Rais Samia ya kuboresha huduma za afya nchini.

Mheshimiwa Spika, natambua kamati imezungumzia maazimio ya viongozi wakuu wa nchi waliyokutana Abuja ya kwamba nchi zinapaswa kutenga asilimia 15 ya fedha zao za bajeti kwa ajili ya afya. Lakini Wabunge naomba tushukuru angalau tunaona ongezeko la fedha za afya kila mwaka. Kwenye hili tutaendelea kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia. Amezungumza Naibu Waziri wangu mafanikio ambayo tumeyapata, majengo yapo kila sehemu, zahanati, vituo vya afya, hospitali za halmashauri tunazungumzia vifaa tiba vya kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miaka miwili iliyopita tulikuwa na CT– Scan 13 tu. Leo tuna CT–Scan 45 ndani ya Rais Samia Suluhu Hassan. Ndugu zangu wa Kigoma leo wana huduma ya CT- Scan, Katavi wana huduma ya CT–Scan, Manyara, Simanjiro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwako Mbeya ninahaidi itakapofika tarehe 30, Juni tutakuwa tumekamilisha MRI na CT–Scan lakini kwenye suala la MRI hajapata tokea. Tulikuwa tuna MRI moja tu Hospitali ya Taifa Muhimbili leo chini ya Rais Dkt. Samia miaka miwili tumefunga MRI Chato, tumefunga MRI Mtwara na tutakamilisha ufungaji wa MRI Mbeya, huyu ndiyo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, maneno machache vitendo vingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu hii miaka miwili iliyopita tukipata wagonjwa mahututi tutawalaza wagonjwa 258 tu. Leo watokee wagonjwa mahututi tuna uwezo wa kulaza wagonjwa 1000 kwa wakati mmoja, huyu ndiye Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumetambua huduma za magonjwa ya dharula (Emergency Medical Department). Mwaka jana 2022 tulikuwa na majengo nane, miaka miwili ya Rais Samia Suluhu Hassan tuna majengo ya EMD 118, tena yameshuka mpaka katika ngazi za halmashauri. Zamani EMD unaiona Muhimbili, unaiona KCMC unaiona Bugando leo mpaka kijijini kule hospitali ya halmashauri unakuta huduma ya EMD. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa huduma za kina mama wajawazito tumeweza kuboresha huduma sasa hivi asilimia 98 ya kinamama wajawazito wana imani na huduma zinazotolewa na wanaudhuria kliniki. Hii imetuwezesha kupunguza vifo vya watoto wenye umri wa chini ya mwaka mmoja kutoka vifo 43 hadi vifo 33 katika kila vizazi hai 100. Lakini vifo vya watoto watano chini ya miaka mitano tumevipunguza kutoka vifo 67 hadi vifo 43. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali ya sekta ya afya duniani inapimwa kwa viashiria hivi. Ikiwemo vifo vya watoto lakini kubwa Tanzania na Dunia ya Kimataifa tulijiwekea malengo, inapofika 2025 watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI wajue hali zao. Leo Tanzania tumefikia asilimia 94.4 kabla ya 2025.

Mheshimiwa Spika, tulipaswa kuweka asilimia 95 ya wenye UKIMWI wanaotumia dawa, wawe wapo kwenye dawa tumeishafika asilimia 95 kabla ya 2025. Lakini habari njema, wanaotumia dawa za kufubaza virusi za UKIMWI asilimia 96 maambukizi ya UKIMWI yamegandamizwa au virusi vya UKIMWI vimepunguzwa nguvu, haya ni mafanikio makubwa chini ya Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nikushukuru sana kwa jinsi unavyoongoza Bunge letu Tukufu pamoja na kusimamia mijadala ndani ya Bunge. Wewe ni icon, wewe ni inspiration kwa wasichana na vijana Tanzania kwamba tunaweza kuwa na wanawake wakafanya kazi kubwa na nzuri kama Dkt. Tulia Ackson hongera sana Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee niwapongeza sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja yetu pamoja na kamati. Kamati yetu madhubuti inayoongozwa na Mheshimiwa Stanslaus Haroon Nyongo Mbunge wa Maswa Mashariki ambaye imesomwa na Mheshimiwa Cecil Mwambe, tumepokea maoni na ushauri wa kamati. Tunawaponeza sana kamati kwa ushauri wenu mzuri lakini kipekee tunawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri kubwa. Kubwa, tutatekeleza maoni naushauri ambao mmetupatia kwa sababu una lengo la kuboresha huduma za afya kwa watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tumefarijika sana kupokea pongezi kutoka kwenu Waheshimiwa Wabunge, pongezi hizi tunazichukulia kama deni letu na watendaji wangu kwenu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wa kufanya kazi zaidi usiku na mchana ili tuweze kuimarisha na kuboresha huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla ya kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge, napenda nitambue Waheshimiwa Wabunge waliyochangia hoja yangu. Wapo Wabunge 47 akiwemo na Naibu Waziri, Wabunge 44 wamechangia kwa kuongea na Wabunge watatu wamechangia kwa maandishi. Kwa sababu ya muda naomba nisiwataje.

Mheshimiwa Spika, hoja kubwa ambazo zimetolewa ziko kama hoja tisa nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kutoa ufafanuzi. Nitajikita katika hoja nane na kama muda utatosha nitazungumzia hoja ndogo ndogo, moja moja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge hoja kubwa ambayo wameileta pamoja na kamati ni Serikali kuwekeza nguvu zaidi katika huduma za kinga badala ya huduma za tiba. Waheshimiwa Wabunge hoja hii tumeipokea na ndiyo maana katika bajeti yangu kipaumbele cha kwanza maana ya huduma za kinga, huduma ya kwanza ya kinga ni chanjo za watoto zinazoweza kuzuia magonjwa. Tumetenga bilioni 114.3 kwa ajii ya kuhakikisha tunatoa chanjo zote za Watoto. Tutanunua pia ma–fridge, majokofu kama 1,600 na tutatumiwa magari ya chanjo 102 na kuyasambaza katika halmashauri zenu ili yaweze kuhudumia suala la chanjo.

Mheshimiwa Spika, chanjo ya pili ambayo tutaipa kipaumbele ni chanjo ya kuwakinga wasichana dhidi ya saratini ya mlango wa kizazi. Waheshimiwa Wabunge, naomba mkawe mabalozi, chanjo hii ni salama, chanjo hii haimzuii msichana kuja kupata mtoto, kuja kupata ujauzito sana sana inamzuia kutokuja kupata maambukizi ya ugonjwa wa saratani.

Mheshimiwa Spika, turuhusu tuje tufanye semina Bunge lako tuonyeshe aina za saratani zinazoongoza kwa watanzania ya kwanza ni sarati ya mlango wa kizazi. Kwa teknolojia hii haikubaliki kuendelea kuwa na kizazi cha wasichana wenye saratani ya mlango wa kikazi. Niwaombe sana wazazi na walezi wenzangu wenye watoto wa umri wa chini ya miaka 14 tuwapatie chanjo ya saratani ya mlango wa kikazi chanjo hii inatolewa bure bila malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia eneo la pili la kinga ni suala la lishe, tutaendelea kuwasaidia wazalishaji wadogo wa chakula, tutawapatia vinu 300 vya kuongeza virutubisho na kutoa matone ya vitamini A kwa watoto wenye umri ya chini ya miaka mitano.

Mheshimiwa Spika, tumeona pia kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi, viwanda vinavyozalisha unga wa ngano, viwanda vinavyozalisha unga wa mahindi, viwanda vinavyotengeneza mafuta ya kula wanapaswa kuongeza virutubisho katika product zao. Kwa hiyo, tutashirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara kuhakikisha viwanda vyote Tanzania vinafanya food fortifications ili tuweze kuimarisha kiwango cha lishe kwa watanzania.

Mheshimiwa Spika, eneo jipya ambalo tunakuja nalo katika suala hili la kinga ni kuimarisha kada ya wahudumu wa afya ngazi ya jamii (Community Healthy Workers). Wamekuwepo hawa watu, mradi wa UKIMWI ana–train wahudumu wa afya ngazi ya jamii siku mbili, watu wa malaria ana–train wahudumu wake wa afya siku tatu, mtu wa kifua kikuu kila mtu anawahudumu wa afya ngazi ya jamii.

Mheshimiwa Spika, tumeona ipo haja ya kuja na mfumo mmoja wa wahudumu wa afya ngazi ya jamii integrated and coordinated community health workers program hawa wahudumu wa afya ngazi ya jamii tutaanza nao elfu tano na Waheshimiwa Wabunge watachaguliwa katika vijiji vyenu na mitaa yenu. Tutazielekeza Serikali za vijiji ndiyo wawachague, tutawapa mafunzo ya miezi sita na tumeamua tujikite katika maeneo makubwa sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ya kwanza ni afya ya uzazi mama na mtoto, eneo la pili litakuwa lishe, eneo la tatu afya na usafi wa mazingira, eneo la nne magonjwa ya kuambukiza hususani malaria, kifua kikuu na ukimwi na eneo la tano magonjwa yasiyo ya kuambukiza hususani ni kisukari, shinikizo la juu la damu na magonjwa ya moyo na eneo la sita ni magonjwa haya ya mlipuko kama Ebola na Marburg.

Mheshimiwa Spika, tunaamini kabisa ameongea Mheshimiwa Oliver pale, tulipata mlipuko wa Marburg kule Goziba kuna watumishi wa afya wawili tu. Ukiweka wahudumu wa afya kila kijiji wawili, watatu wale ndiyo watakuwa jeshi la kwanza la afya la kuwafikia wananchi kutoa huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, nimepokea concern kuna wahudumu wa afya ngazi ya jamii waliyopo, waliosoma siku mbili, wiki moja, wiki tatu hatutawaondoa tutawa–phase out kidogo kidogo. Kwa hiyo, hii niwatoe wasiwasi kwa hawa tuna–train, tutawalipia lakini hawa wataendelea lakini baada ya muda tutawaondoa kidogo kidogo.

Mheshimiwa Spika, eneo la nne kwa upande wa kinga ni suala ya afya mazingira. Tutaanzisha kampeni ya usafi wangu mita tano, mita tano usafi wangu lakini pia tunafikisha miaka 50 ya kampeni ya mtu ni afya iliyoanzishwa na Rais wetu Julius Kambarge Nyerere. Katika kufanikisha huduma za afya, mazingira tutawabana sana Serikali za mitaa watekeleze sheria ndogo zinazosimamia usafi na afya mazingira.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni ubora wa huduma, Wabunge wengi hapa wamesema mmejenga majengo, mmeleta vifaa tiba lakini huduma siyo nzuri. Tunakubaliana na Waheshimiwa Wabunge, kwamba uwekezaji mkubwa uliyofanywa na Serikali katika eneo la miundombinu, vifaa vya uchunguzi na vifaa tiba pamoja na kuajiri watumishi lakini bado kuna baadhi ya hospitali zetu hazitoi huduma bora.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge tumebaini kuwa changamoto kubwa ni uongozi. Jana nilitoa mfano wa Hospitali ya Muhimbili chini ya Profesa Janabi, ni uongozi. Kwa hiyo tunakuja na programu ya mabadiliko ya kiutendaji kwa wasimamizi wa utoaji wa huduma za afya (Leadership for Health Transaformation Program) ili kuwaongezea uwajibikaji, ufanisi na tija katika utoaji wa huduma za afya. Lakini tutaimarisha utawala bora, uongozi na menejimenti za usimamizi za hospitali, kwa kushirikisha kamati za ulinzi na usalama za wilaya na mikoa. Lakini tutafanya kaguzi za mara kwa mara na za kushtukiza ili kuimarisha usimamizi shirikishi katika vituo vya kutoa huduma za afya. Vile vile tutaendelea kushirikiana na mabaraza ya kitaaluma kuhakikisha wanataaluma wao wanatoa huduma bora za afya.

Mheshimiwa Spika, tumeanzisha pia kwenye mitaala ya vyuo vya afya somo la customer care. Kwa hiyo shule na vyuo vyetu vya afya pia vitafundisha masuala ya good customer care, matumizi ya lugha ya staha na faraja kwa magonjwa, ili wanaomaliza pia wasiwe tu wanatibu lakini pia wafanye huduma kwa kutumia lugha nzuri.

Mheshimiwa Spika, suala la rasilimali watu katika sekta ya afya, uhaba wa watumishi limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge zaidi ya kumi. Sisi tumeendelea kuajiri watumishi takribani 100,000. Sekta ya afya inahitaji watumishi takribani 219,000 na waliopo ni kama 109,616. Sambamba na kuomba vibali utumishi sisi wenyewe kama sekta ya afya tumejiongeza kwa hospitali zetu kupitia mapato yao ya ndani kuajiri wataalamu wa afya takribani 4,189 ambao wameajiriwa kwa mikataba. Lakini pia kuanzia mwaka jana nimewataka wadau wote wa maendeleo wanaotekeleza miradi ya afya nchini, kutumia angalau asilimia 10 ya fedha zao kuajiri watumishi wa afya. Badala ya mradi malaria sijui malaria kila baada ya dakika moja kwenye redio na Tv, tunakata asilimia 10 ya fedha za miradi zinakwenda kuajiri watumishi wa afya na tutawapeleka katika maeneo ambayo yana uhaba. Lakini pia tutatoa mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu ya wataalamu wa afya, hususani madaktari bingwa na bobezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumetangaza juzi ajira za madaktari bingwa 30. Mpaka tunafunga muda tumepokea maombi ya madaktari bingwa 12 tu. Kwa hiyo madaktari bingwa wengi wanapenda kufanya kazi katika sekta binafsi. Tulichokiona, sera inataka tusomeshe madaktari bingwa walioajiriwa na Serikali, inatutaka tusomeshe watumishi walioajiriwa na Serikali; lakini tumeangalia katika hospitali zetu kuna watumishi wanaojitolea zaidi ya miaka miwili hadi miaka mitatu. Kwa hiyo hao tutawapeleka kusomea udaktari bingwa na tutawapa mikataba ya kufanya kazi katika hospitali husika angalau kwa muda wa miaka minne ndipo wanaweza Kwenda kwenye hospitali binafsi. Suala hili pia nadhani uliligusia wakati wa maswali na majibu.

Mheshimiwa Spika, eneo jingine ni kuhusu magonjwa yasiyo ya kuambukiza. Tutaendelea kutoa elimu kwa jamiii kuhusu magonjwa yasiyo ya kuambukiza, tutafanya utafiti. Mwaka huu tunafanya utafiti wa kitaifa; na kwa upande wa elimu ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge naomba niwahamasishe, mambo manne tu ukiyazingatia. Ya kwanza, mazoezi angalau zisipungue dakika 30 kwa siku, moyo uende mbio na utoke jasho. Pili, punguzeni matumizi ya chumvi kupita kiasi. Tatu, punguzeni matumizi ya sukari na unaweza kuishi bila kula sukari; kama ulikuwa unatumia vijiko vitatu tumia kijiko kimoja. Vilevile eneo la nne ni kupunguza mafuta na sisi Wizara ya afya tumepeleka maombi kwa Wizara ya fedha kuangalia jinsi gani wanaweza kuongeza ushuru kwenye bidhaa hizi ili tupunguze matumizi ya bidhaa zinazosababisha magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza. Tutajikita kwenye magonjwa matatu; kisukari, shinikizo la damu pamoja na magonjwa ya moyo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza pia tumeshusha huduma hizi tumeanzisha kliniki katika ngazi za msingi, lakini pia tutaanzisha vituo 100 vya uchunguzi wa saratani katika ngazi ya msingi.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la huduma za utengamao (rehabilitative services). Asubuhi hapa nimemtambulisha mwanangu Lukiza. Lukiza sijui kama unanisikia Lukiza. Nadhani mnamuona ndivyo yuko hivyo. Lukiza amezaliwa na tatizo la autism, usonji. Lukiza alikuwa hawezi kuvaa nguo, hawezi kula, hawezi kupiga mswaki, hawezi kufanya chochote. Mama yake Hilda amehangaika na mtoto. Lakini kwa sababau ya huduma za utengamao ikiwemo huduma za mazoezi tiba, huduma za kazi (occupational therapy), huduma za speech, Lukiza anaweza kujivalisha nguo zake mwenyewe leo, Lukiza anaweza kula leo, Lukiza ametulia pale ameingia saa kumi, Lukiza hajafanya fujo yoyote kwa sababu amefundishwa jinsi ya kufanya utulivu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala hili limenigusa kama mama. Ukienda kwenye vituo vya watoto wenye ulemavu asilimia 99.5 wanapelekwa na akina mama wenzangu. Sisi kama Serikali tumeamua kuimarisha huduma za utengamao kwa watoto lakini pia tunaboresha huduma hizi kwa sababu umri wa kuishi pia unaongezeka wazee nao wanakua. Lakini pia ajali zimeongezeka, Profesa Ndakidemi umesema hapa mtu amekatwa mguu, amekatwa mkono, huduma za utengamao ndio zinamsaidia mtu tuishi maisha bora (quality life). (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile pia tutaangalia watoto wenye autism, tutaangalia watoto wenye mtindio wa ubongo, watoto wenye udumavu wa akili, watoto wenye mongolia, watoto wenye ukosefu wa utulivu. Waheshimiwa wabunge anaweza akazaliwa mtoto ana ukosefu wa utulivu akapewa masaa mawili atunge ushanga, miaka miwili mtoto yule anabadilika anakuwa na utulivu. Kwa hiyo eneo hili ni eneo ambalo tutalipa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, na kipekee nimpongeze sana Hilda Nkabe kama mama, akaanzisha taasisi ya Lukiza Autism Foundation ili kuongeza elimu na hamasa ya watoto wenye usonji. Lengo la Hilda ametaka wanawake wenzake wasiwafiche watoto wenye usonji na watoto wenye ulemavu. Ndiyo maana kila mwaka tunafanya mbio (Run for Autism) ili kuongeza hamasa kuwaonesha kwamba watoto hawa wanawezekana.

Mheshimiwa Spika, nipongeze wataalamu wetu. Tunaye Doctor ambaye amekuja hapa mtaalamu wa Physiotherapy, Godfrey Kibati, ambaye anafanya masuala la Occupational Therapy. Tutashirikiana naye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona mpaka twende Muhimbili hawa madaktari wakasome miaka mitano hatutafika. Kwa hiyo tutaanzisha kozi za miezi sita mpaka tisa za muda mfupi. Tuchukue wauguzi labda wawili kutoka kila hospitali au kila halmashauri, madaktari wawili kutoka kila hospitali kila halmashauri tuwapeleke wasome angalau kozi hizi tatu za masuala la tiba utengamao.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumesema, kwamba lazima tufanye assessment. Tiba hizi za utengamao zinapatikana wapi? Kwa hiyo tutafanya assessment kujua vituo vyote ambavyo vinafanya huduma hii, ikiwemo kuimarisha huduma za matibabu. Lakini pia kuna suala la afya ya akili na namna ya kukabiliana nalo. Tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kuona umuhimu wa Serikali kuwekeza kwa kuibeba ajenda hii ya afya ya akili. Afya ya akili ndio msingi wa afya ya binadamu. Hakuna afya bila afya ya akili, na ndio uchumi wa mtu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwenye hili, kama ilivyo kwenye huduma za utengamao, hatuna wataalamu wa kutosha. Tunafurahi wenzetu wa Chuo Kikuu cha Muhimbili (MUHAS) mwaka huu wataanzisha kozi ya Clinical Psychology, angalau, na mimi nimewaambia, sisi Serikali tuko tayari kugharamia wanafunzi 10 watakaofanya degree ya kwanza ya Clinical Psychology ili tuweze kuwapata na kuwasajili katika maeneo mbalimbali. Lakini tunatoa elimu kwa umma kuhusu vihatarishi vya afya ya akili na namna ya kukabiliana nayo. Tutahakikisha pia kwamba tunakuwa na wataalamu wa muda mfupi, maana tukisubiri wamalize miaka mitano tutakuwa tumechelewa sana. Kwa hiyo hii pia tutaifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tumeamua kuipandisha hadhi Hospitali ya Taifa ya Akili Mirembe, itakuwa ni Taasisi ya Taifa ya Afya ya Akili. Tunawataka Mirembe wafanye promotional activities, wafanye tiba, wafanye mafunzo na wafanye tafiti. Kwa hiyo tutawapa maeneo makuu manne. Vilevile pia tumesema tutaanza na huduma za afya ya akili katika hospitali kumi za rufaa za mikoa na hospitali za halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kuhusu umuhimu wa kuanzisha huduma ya kisaikolojia Balozi dada yangu Jesca Msambatavangu ameiongea vizuri. Tunawaaalika sekta binafsi; Ulaya, Marekani, India hii ni biashara kubwa. Yoga masuala ya rehabilitation, masuala ya breathing technique, kama kuna mtu kuna msitu mzuri akaanzishe watu waende siku mbili wakaondoe ma-stress ya Bungeni, muondoe ma- stress ya familia nyumbani, baba amekuchukiza, jamani Watanzania tengeni muda wa ku-refresh, otherwise mtapata changamoto nyingi. Kwa hiyo suala hili tutaendelea kuliboresha.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto, kwa kweli tunakwenda vizuri. Lakini jambo moja ambalo limezungumzwa na Wabunge wenzangu wananwake, wameniuliza, Mheshimiwa Waziri, hebu tuambieni sasa sera ya huduma hizi ni bure au siyo bure? Nimefanya uchambuzi na timu yangu, tukaangalia, Mheshimiwa Waziri wa fedha yupo. Tukaangalia mama anatakiwa kwenda kliniki angalau mara tano wakati wa ujauzito. Hudhurio la kwanza ni shilingi 2,397. Hudhurio la pili shilingi 15,187. Hudhurio la tatu 2,397. Hudhurio la nne 1,727. Hudhurio la tano ni 2,397. Kwa hiyo kwa mahudhurio matano mwanamke mjamzito gharama ni shilingi 24,103. Tumeondoa umeme, tumeondoa mzani, tumeondoa dawa ambazo zinanuliwa na Serikali, hizi ni zile re-agent kufanya nini kwa mfano, Hb, kupima wingi wa damu, protini, kupima mkojo pamoja na kupima blood glucose. Tuna wanawake takribani milioni mbili kila mwaka, kwa hiyo ni 48,000,000,000.

Mheshimiwa Spika, tukienda kwenye huduma za kujifungua kawaida, tumefuta vitu vidogo vidogo vingine vyote, tumepata ni 32,952. Wanawake 1,600,000 ndio wanajifungua kawaida, kwa hiyo inakuwa kama 52,000,000. Wanaojifungua kwa upasuaji gharama ni 63,000; kwa hiyo hapa inakuja bilioni 119. Hivyo, kama tunataka kutoa huduma bora kwa wanawake wajawazito Waheshimiwa Wabunge ni bilioni 119, hatujaweka umeme, hatujaweka maji, hatujaweka vifaa, hatujaweka CT-scan, hatujaweka X- Ray mashine, hatujaweka ultrasound. Kwa hiyo tunaongea na wenzetu wa Wizara ya fedha, kwamba hebu watuangalie huko mbeleni kama kuna elimu bure basi na hili sasa liende badala likabaki kwenye makaratasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hiyo ndiyo gharama ambayo tumeipata. Lakini niendelee kusisitiza kwa watoa huduma za afya. Kuna dawa tunazinunua bure, nataka wajawazito wapewe bure. Kuna vitu tunavinunulia bure, tunataka wajawazito wapewe bure.

Mheshimiwa Spika kuna suala la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya. Kabla sijazungumza hili niende kwenye kuimarisha huduma za ubingwa bobezi. Kwenye hili kwa kweli tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kutambua mchango wa wataalamu wetu. Lakini kipekee tunamshukuru Rais Samia, tumetenga safari hii bilioni 23, amesema Naibu Waziri. Kupeleka mgonjwa wa figo nje ya nchi ilikuwa milioni 120 lakini ndani ya nchi milioni 30. Uroto nje ya nchi milioni 250 na ndani ya nchi ni milioni 58 mpaka 70. Kwa hio ilikuwa ni kukosea niliposema bilioni kwa hiyo ni milioni 58.

Mheshimiwa Spika, tulikaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha, tukampelea Mheshimiwa Rais maombi yetu. Kama mgonjwa huyu mtoto wa sickle cell anaweza kupona kwa milioni 58 kama tulikuwa tunapeleka wagonjwa hawa nje ya nchi kwa nini tiusitenge fedha ya ndani ya kuwasaidia wasio na uwezo kupata huduma hizo. Tunamshukuru Rais Samia, na ndiyo maana bajeti yetu ina addendum. Tumepata bilioni tano za kugharamia kupandikiza uroto kwa watoto wenye sickle cell, lakini pia tutapandikiza figo kwa watu wenye matatizo ya figo, na eneo la tatu tutapandikiza watoto vifaa vya kusaidia kusikia cochlear implants. Tutaweka vigezo, tangu jana tulivyosema nimepata maombi mengi, kwa hiyo tutaweka vigezo yupi atastahili, yupi hatastahili. Lakini kubwa Waheshimiwa Wabunge wataalamu wetu wanafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa tiba utalii, hapa ninaposema wataalamu wetu saba wameitwa Malawi ili kutoa huduma za uchunguzi wa moyo kutoka Jakaya Kikwete na wameshawachunguza wagonjwa 720, na kati yao 537 wamegundulika kuwa na matatizo ya moyo, wanakuja Tanzania kupata huduma hii. Kwa hiyo tiba utalii itakuwa inawezekana chini ya Rais Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalize hili la bima ya afya. Bima ya afya ndiyo roho ya huduma za afya nchini. Asilimia 70 ya fedha za hospitali zetu za umma na binafsi zinategemea bima ya afya. Tumefanya actuarial studies na kuona kwamba baadhi ya vifurushi vinahatarisha uhai na uendelevu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya. Ndugu yangu Hawa ameliongea. Hawa Toto Afya Card anachangia 50,400. Katika kila shilingi 100 wanatumia shilingi 667. Lakini la pili tumefanya uchambuzi zaidi, katika mwaka 2021 watoto waliosajiliwa Toto Afya Card walikuwa 157,920 wakachangia bilioni 5.9 wakatumia bilioni 40.5; jamani kuna bima ya afya hapo? Unachangia bilioni tano unatumia bilioni 40.

Mheshimiwa Spika, fedha zinaenda wapi? Asilimia 53 kumuona daktari. Watanzania tuna utamaduni fulani hivi. Nikishakuwa na bima ya afya kitu cha kwanza naenda kwenye polyclinic ya kumuona specialist; tukaangalia magonjwa gani haya. Ugonjwa wa kwanza ni malaria, malaria unatibiwa katika zahanati. Ugonjwa wa pili mfumo wa hewa, unatibiwa katika ngazi ya zahanati, ugonjwa wa tatu UTI. UTI inatibiwa katika ngazi ya chini. Kwa hiyo tumeangalia hela asilimia 58 za hela ya Toto Afya Card zimeenda kwenye vituo binafsi vya kutoa huduma za afya, asilimia 20 imekwenda hospitali za Serikali, asilimia 22 imekwenda katika vituo vya taasisi za dini. Kwa hiyo mtaona wenyewe hakuna uendelevu wa bima ya afya ya Toto Afya Card.

Mhesimiwa Spika, sasa, the way forward mtu-challenge, the way forward, ndiyo maana tunasema kuna vifurushi, kwamba watoto wasajiliwe Pamoja na wazazi wao. Lakini la pili watoto wasajiliwe wakiwa shuleni. Kama kuna watoto 100, kwa sababu kama shule ina watoto 100 watakaoumwa watakuwa labda 10 watasaidia 90 watalipia wenzao 10 watakaoumwa, lakini hili suala the way forward yake ni bima ya afya kwa wote. Bima ya afya ndiyo itakayotutoa.

Mheshimiwa Spika, tumefanya uwekezaji mkubwa katika huduma za afya, tumejenga ili wananchi wapate huduma bora za afya, inabidi waweze kulipia kabla ya kugua. Suala hili tunaendelea na majadiliano ndani ya Kamati, tunaamini tutaweza kufikia muafaka.

Mheshimiwa Spika, maswali mengine mojamoja ambayo ni suala la dada yangu Mheshimiwa Fatma Toufiq kuhusu Health Basket Fund ipelekwe kwenye dawa. Asilimia 33 ya hela ya Health Basket Fund inapaswa kutumika kwa ajili ya dawa, lakini tunazungumza kuijengea mtaji MSD. Hapa tunalalamika MSD haipeleki dawa, tutabadilisha watu kama hatutaipa mtaji MSD ikawa ni duka, ukishakuwa na vifaa vyako una-order unapewa. MSD sasa hivi anasubiri hela za vituo zije ndio akanunue dawa.

Mheshimiwa Spika, la pili, suala la dada yangu Mheshimiwa Munde, tumewanyang’a, kwa nini Hospitali ya Kanda imetoka Tabora imepelekwa kwingine. Hatujawanyang’anya tuliangalia vipaumbele. Tuliona Kigoma tutavutia DRC, wagonjwa wa Burundi na wagonjwa wa Rwanda, ndio maana tukaenda Kigoma, lakini nataka kuwapoza, tutajenga Hospitali ya Taifa ya Huduma za Watu Wenye Ulemavu Tabora kwa sababu, walishatenga eneo. Hilo jambo tunataka kuwaahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalize kuhusu majengo yote ambayo hayajakamilika. Tumetenga fedha na tumekubaliana ndani ya Wizara, badala ya kuanza ujenzi mpya ni vizuri tukakamilisha ujenzi wa majengo ambayo tumeyaanza.

Mheshimiwa Spika, la mwisho ni huduma kwa wazee. Huduma kwa wazee tumelipokea na tumeanza. Dawa za kisukari aina mbili za wazee sasahivi zitapatikana katika ngazi ya zahanati. Dawa aina tano za kisukari kwa ajili ya wazee na magonjwa yasiyo ya kuambukiza, tumezishusha kutoka Hospitali ya Wilaya, sasa zitapatikana katika kituo cha afya, lakini pia tutaendelea kuimarisha.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema kwamba, tumepokea hoja za Wabunge zote na nyingine tutazijibu kwa maandishi ikiwemo upatikanaji wa ambulance, amesema vizuri Naibu Waziri wangu. Tulipokwenda Toyota basic ambulance walitupa bei ya milioni 144, tukaenda UNICEF tukapata kwa milioni 83.9, advanced ambulance, Toyota, sijui kama naharibu biashara ya mtu sijui lakini, tukapewa bei ya shilingi milioni 162, tukatumia UNICEF tumepata kwa shilingi milioni 93. Kwa hiyo, tume-save bilioni 17.8, amesema hapa Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kila halmashari itapata ambulance mbili na sisi Wizara ya Afya tutaongeza ambulance moja kwa baadhi ya majimbo ambayo yana idadi kubwa ya vifo vya akinamama wajawazito na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalize tu kwa kusema, hospitali zetu hizi…

SPIKA: Dakika moja, malizia Mheshimiwa.

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nimalize kwa kusema, niwaombe sana tuilinde NHIF. Muhimbili JKCI ya Jakaya Kikwete, hela anazokusanya cash ni bilioni 5.0, NHIF analipa bilioni 22 kwa mwaka. Muhimbili, hela anayokusanya cash bilioni 12, NHIF bilioni 50; hela hizi ndivyo wanavyotupa maombi, nina mgonjwa amekwama Muhimbili, nina mgonjwa amekwama JKCI, nadaiwa maiti, ndio zinatumika kulipia wagonjwa wetu.

Mheshimiwa Spika, nimalize kwa kukushukuru wewe, lakini pia kwa kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa ushirikiano mkubwa anaonipatia. Katibu Mkuu Dkt. Seif Shekalaghe, Naibu Katibu Mkuu Dkt. Grace Magembe, Wakurugenzi wote wa hospitali, lakini kipekee nimshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini kuwa Waziri wa Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge, hii ni bajeti yangu ya saba kusoma kama Waziri wa Afya. Mwaka huu tutaleta mabadiliko makubwa zaidi ili tuweze kuboresha huduma za afya. Sio kwamba, najua sana au nina akili sana, lakini naamini ni kwa sababu ya kudura na kadari za Mwenyezi Mungu. Ndio maana nasimama hapa kwa mara ya saba kusoma bajeti ya Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru familia yangu, ndugu zangu na watu wangu wa Tanga Mjini, nawapenda sana. Watu wa Tanga waangalie kazi zangu za Tanga Mjini, tumejenga barabara, tumejenga shule, tumeboresha Bandari ya Tanga, tumefanya mikopo. Naamini 2025 Tanga Mjini wanarudi na Odo Ummy Mwalimu na sio mtu mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Muswada wa Sheria ya Madaktari, Madaktari wa Meno na Wataalam wa Afya Shirikishi wa Mwaka 2016
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nianze kuwashukuru wachangiaji wa hoja hii ya Muswada wa Sheria ya Madaktari, Madaktari wa Meno na Wataalamu wa Afya Shirikishi; namshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Mheshimiwa Peter Serukamba, Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, Mheshimiwa Mussa Mbarouk na Mheshimiwa Dkt. Godwin Mollel.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia namshukuru sana Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla kwa michango yao. Vile vile namshukuru sana Mheshimiwa Lucia Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum ambaye pia ametuletea mchango wake kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kujibu hoja zilizotolewa mbele ya Bunge lako Tukufu, kwanza nirudie kusema ni kwa nini tumekuja na muswada wa sheria hii? Kubwa tuna ongezeko la wataalamu, wale wenyewe tu Madaktari na Madaktari wa Meno wanaongezeko kama alivyosema Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano tulikuwa tunazalisha madaktari chini ya 100, lakini sasa hivi Tanzania ni moja ya nchi zinazosifika kwa kuzalisha idadi kubwa sana ya madaktari. Tunazalisha madaktari zaidi ya 1,000 kwa mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeonyesha kwamba zipo sasa kada au taaluma nyingine muhimu ambazo zinahusiana moja kwa moja au ni muhimu sana katika utoaji wa huduma za afya. Sheria hii ilikuwa inaangalia tu Madaktari, Madaktari wa Meno na inawaacha kwa mfano watu wa physiotherapy ambao ni muhimu sana siku hizi, watu wa lishe, wale watengeneza viungo bandia na watu wa matibabu ya afya ya akili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunachotaka kukifanya sasa, tunakuja na sheria moja ambayo itasimamia kwanza taaluma, pili maadili ya wataalamu hawa na watoa huduma za afya. Lengo letu ni nini? Ni kutaka kulinda afya na usalama wa Watanzania. Hilo ndilo lengo kubwa ambalo limetufanya tulete sheria hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikienda katika hoja zilizotolewa na Kamati, kimsingi napenda kusema kwamba tumekubaliana kwa kiasi kikubwa na ushauri ambao umetolewa na Kamati. Kwa mfano, suala ambalo walikuwa wamelieleza kwenye kifungu cha tatu, kwenye ufafanuzi (interpretation), mabadiliko makubwa ambayo tumeyafanya
kwenye muswada huu tulikuwa tukisema Medical Practitioner tunasema ni yoyote ambaye ana digrii ya medicine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tunatambua mtu ambaye ana certificate, diploma, advanced diploma au degree kwenye medicine naye ni Medical Practitioner. Kwa hiyo, tumewaingiza wote kwenye tafsiri hiyo. Nafurahi sana kuona sasa tumeweza kupunguza joto lililokuwepo Mtaani. Jambo la pili kwenye Allied Health Professionals, tumeamua pia kwamba yeyote ambaye ana certificate, diploma, advanced diploma au degree kwenye hizo Allied Health Professional naye ataingia kwenye kwenye kundi moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kubwa ambalo tumelifanya kwenye jedwali la marekebisho; iwapo ni mtu katika fani ya tiba ya medicine au katika allied health professional ana degree, hawa tumewaweka kwenye sehemu moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutakuwa na registrar ya wanataaluma wa Medicine, Dental na Allied Health Professionals, wataingia pale. Kwenye role, Medical, Dental na Allied Health Professional ambapo mtu ana Diploma au Advanced Diploma ataingia pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwenye schedule of ammendment, kwenye lile jedwali la tatu kuna maneno yameachwa. Kwenye list pale inatakiwa itangulie na Medical, Dental and Allied Health Professional, lakini pia kwenye role. Kwa hiyo, tumeweka utaratibu mzuri. Lengo letu ni nini? Tunafikiria hata kuanzisha role ya specialist ili watu tuwachochee watu waweze kutaka kuongeza ujuzi zaidi kutaka kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nataka kulitolea ufafanuzi na limeongelewa pia na Msemaji wa Kambi ya Upinzani na Kamati ya Kudumu ya Bunge, ni suala la madaraka au mamlaka ya Baraza la Madaktari. Kabla sijaenda kwenye Baraza, wamezungumzia suala la Msajili kwamba ateuliwe kutoka nje. Huu ni ushauri kutoka kwa Msemaji wa Kambi ya Upinzani. Tunaukataa ushauri huu kwa sababu tunazo taratibu zetu za kuteua Wasajili kwa kuzingatia Sheria za Utumishi wa Umma. Kwa hiyo, tutazingatia taratibu za uteuzi katika Utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ni suala la Baraza. Tunafurahi, tumekubaliana na ushauri wa Kamati na Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwamba walitushauri tuongeze idadi ya Wajumbe. Tumeongeza idadi ya Wajumbe kutoka saba, tumeweka Wajumbe tisa. Pia tumesema awepo na Mjumbe ambaye atawakilisha watu wenye ulemavu kutoka kwenye vyama vya wanataaluma.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine kubwa mbalo limechangiwa na Mheshimiwa Nyongo, Mheshimiwa kaka yangu Mussa Mbarouk Mbunge wa Tanga ni suala la nidhamu na maadili ya daktari na ndiyo maana tumekuja na sheria hii. Tutawabana na kuwasimamia Madaktari, Madaktari wa Meno na Wataalamu wa Afya Shirikishi kwa kutumia sheria hii. Kwa hiyo, wale ambao watakuwa wanafanya kazi vichochoroni bila leseni maana yake ni kwamba mara tu baada ya Mheshimiwa Rais kusaini sheria hii, sisi tutaanza mara moja kuchukua hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna mtindo sasa hivi watu wanatoka nje wanakuja kushika wagonjwa wetu bila kufuata taratibu zinazohusika. Kwa hiyo, ni jambo ambalo tutakuwa wakali sana kwa sababu tumepewa dhamana ya kusimamia maisha na afya za Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kaka yangu Mussa kwenye suala la maadili kama anavyosema, hili kwa kweli nataka kulitolea maelekezo. Ni kweli nataka kukiri, unakwenda kwenye hospitali au Kituo cha Afya cha Serikali halafu daktari anakwambia, unajua ukija kwenye kituo changu fulani utapata huduma bora zaidi. Hatutakubali, tutamchukulia hatua mtu yeyote ambaye atakuwa badala ya kutoa huduma nzuri zenye ubora, wakati anafanya kazi katika vituo na taasisi za umma, anao wajibu huo wa kuhakikisha anatoa huduma bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria hii ikipita ndiyo itakuwa kibano chetu. Moja ya mambo makubwa ambayo tutayafanya, tutafuta leseni kwamba hatafanya private wala kwenye government.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitoe rai na Mheshimiwa Naibu Waziri amelisema, madaktari na watoa huduma wengi wa Tanzania wanaofanya katika Serikali ni watu wanaojituma, ni watu wazuri. Kwa hiyo, kuna mambo inapotokea kesi tumhukumu mtu mmoja, kwa mfano, unasema wauguzi wa Dodoma General wabaya, hapana. Tunasema taja Daktari Ummy Mwalimu, Dkt. Hamisi Kigwangalla, muuguzi fulani fulani. Kwa hiyo, hilo ni jambo ambalo muswada huu ukiwa sheria tutaweza kulisimamia. Na mimi nitumie fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza madaktari wote, matabibu na madaktari wasaidizi kwa kazi nzuri wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua kuna changamoto ya uhaba wa watumishi. Badala kazi kufanywa na madaktari sita, utakuta wako watatu. Kwa hiyo, hili Mheshimiwa Mussa tusiwalaumu tu pia tuangalie na changamoto ambazo wanakabiliana nazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Dkt. Mollel alileta suala la Bima ya Afya kwa Madaktari na limetolewa pia na Kamati ya Kudumu ya Bunge. Nikisoma kifungu cha 6(a) cha sheria inayopendekezwa, inazungumzia kwamba Baraza litakuwa na mamlaka ya kumshauri Mheshimiwa Waziri katika utendaji kazi wa Madaktari, Madaktari wa Meno na Wataalam wa Afya Shirikishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sidhani kama suala la bima ni jambo zuri kuliweka hapa kwenye sheria. Tunakubaliana kwamba ni muhimu, lakini tuliache lije kwa kutumia mgongo kutoka kwenye Baraza la Madaktari, maana lile ndilo litakuwa Mshauri Mkuu wa Waziri, siyo masuala ya bima, lakini katika masuala mazima ya maslahi na motisha kwa Madaktari, Madaktari wa Meno na Watoa Huduma za Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Stanslaus Nyongo alizungumzia suala la Continuous Professional Development (CPD). Ni suala kubwa sana na pia ndiyo lengo kubwa la kuja na Muswada huu. Hatutaki tu iwe kwamba, ukishapata certificate yako kutoka Muhimbili, Kairuki Hospital University au Bugando then tayari umekuwa ni professional. Kwa hiyo, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri, sisi tutafanya, wasome kote, tunafikiria kuja na mtihani mmoja kokote utakakosoma, hatutakuruhusu uguse mgonjwa wetu bila kuwa umefaulu mtihani utakaotolewa na Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo tutalifanya ni kwamba, watakuwa wana-renew license zao kama wanasheria wanavyofanya, kwamba kila mwaka una- renew license yako ya ku-practise. Angalau hatutasema hela nyingi, lakini maana yake, itamfanya sasa mwanataaluma atake pia kujiendeleza zaidi na zaidi. Hii kwa kweli nakishukuru sana Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), wanaliunga mkono sana suala la Continuous Professional Development. Kwa hiyo, tutakaa nao na tuweze kuliwekea utaratibu maalum wa kwenda nalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati pia ilitushauri suala la kuondoa ile temporary registration kwa mtu ambaye ametoka nje. Tumelikubali kwa kiasi kikubwa kama nilivyosema. Pia Kamati ilitushauri tuhakikishe tunaweka vizuri ili mtu aweze kuingizwa kwenye hiyo register, orodha au list ya Madaktari, Madaktari wa Meno na Wataalam wa Afya Shirikishi walete vitu gani, yote tumeyazingatia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme jambo lingine ambalo limezungumzwa na Mheshimiwa Nyongo kwamba Kamati iweze pia kuwaingiza hadi Clinical Officers and Assistant Medical Officers. Medical Association of Tanzania (MAT) is registered under Societies’ Ordinance. Kwa hiyo, it is a voluntary, siyo kitu cha lazima. Kwa hiyo, wenyewe watakavyoona kama kuna haja ya kuwa-invite hawa as associate members, hiyo haina shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwetu sisi kama Serikali, ndiyo maana tumeingiza kwenye hili Baraza jipya (Medical Council of Tanganyika). Waheshimiwa Wabunge mnaweza kuuliza, kwa nini mmeendelea kuli-maintain hilo jina?

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kutokana na historia yake, tuendelee kuli-maintain. Kwa hiyo, kwenye Medical Council of Tanganyika ndipo sasa wawakilishi wote wa wanataaluma hawa wataweza kupata uwakilishi kama nilivyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani nimemaliza karibu yote. Kuhusu uteuzi wa Msajili kwamba uanzie kwenye vyama, nimeshalijibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani tuko vizuri, lakini kuhusu muswada, niende sasa kwenye mambo makubwa matatu ambayo yameongelewa na Msemaji wa Kambi ya Upinzani, kuhusu suala la dawa, vifaa na vifaa tiba. Msemaji wa Kambi ya Upinzani na Watanzania watusikilize. Haijawahi na haijapata kutokea katika historia ya Tanzania, Serikali kuwekeza fedha nyingi sana kwenye dawa, vifaa na vifaa tiba. We are on the right track, juzi nilikuwa kwenye mkutano, watu hawaamini nilipowaambia bajeti ya dawa ya Serikali imetoka 31 billion mpaka shilingi bilioni 251 na sasa hivi tunazungumzia shilingi bilioni 269. Haijawahi kutokea. Nchi nzima ilikuwa inaendeshwa kwa fedha za dawa shilingi bilioni 24 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeanza mwaka wa fedha 2017/2018 ninasimama kwa fahari. Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli ametupa shilingi bilioni 23 kwenye first quarter kwa ajili ya dawa, vifaa na vifaa tiba. Kwa hiyo, tunazo changamoto, lakini lazima pia mkubali, mu-appreciate jitihada kubwa ambazo Serikali ya Awamu ya Tano inafanya katika kuimarisha upatikanaji wa dawa, vifaa na vifaa tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, Naibu Waziri amesema, tunaenda kufunga PET-Scan pale Ocean Road, tutapunguza rufaa nje ya nchi (referral abroad) kwa zaidi ya asilimia 50.

Hakuna Kenya, haipo Uganda, haipo Malawi, haipo Zambia, haipo Burundi, haipo Rwanda, itakuwepo Tanzania na chini ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli, inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la universal health coverage. Tunakubaliana nanyi kwamba ni jambo muhimu ambalo tunatakiwa tuliwekeze.

Waheshimiwa Wabunge, natarajia kuja Bungeni kuleta Muswada ambao utamlazimisha kila Mtanzania kuwa na Bima ya Afya. Hiyo ndiyo njia ambayo itatutoa Watanzania, kwa sababu ni bora tuchangiane shilingi 10,000 kwa kila kaya, badala ya wachache mpaka uumwe ndiyo ukatoe shilingi 30,000 au shilingi 50,000. Universal Health Coverage (Bima ya Afya kwa Kila Mtu) ndiyo itawezesha kila Mtanzania kupata bima bora za afya bila vikwazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la dawa ambalo nami nalipokea kutoka kwa Msemaji wa Upinzani, ni kwenye zile orodha 135, kwenye ile aina ya dawa 135 tumeshatoa maelekezo kwa wataalam kwamba wazipitie waone kama tutaongeza zaidi zifike 200 mpaka 250 katika ngazi ya MSD. Pia tumeshatoa maelekezo kwamba hata zile dawa ambazo tunazipima kwenye vituo vya kutoa huduma za afya (Tresor Medicine) ambazo ziko aina 30 na zenyewe tunafikiria kuziongeza kwa kuangalia hali halisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unapo-compare kwamba hospitali binafsi zina dawa, ni kutokana na mazingira ambayo yalikuwepo. Sasa hivi na kwa taarifa yako, Muhimbili ilikuwa inapata shilingi milioni 200 tu kutoka bima, sasa hivi anakusanya shilingi bilioni mbili kwa mwaka. Kutoka shilingi milioni 200 mpaka shilingi bilioni mbili kwa mwaka. Watanzania wana imani na huduma zinazotolewa katika vituo vyetu vya umma, ikiwemo Hospitali ya Muhimbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sitaki kupigiwa kengele, lakini niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kuchangia hoja hii. Namshukuru sana Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na timu yake, wamefanya kazi kubwa na nzuri. Naishukuru Kamati ya Bunge, namshukuru Naibu Waziri, Chief Whip wetu na wote ambao wamefanikisha kuweza kukamilika kwa msaada huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo sasa, sisi tupo tayari kwenda mbele kusimamia Madaktari, Madaktari wa Meno na wanataaluma wa afya shirikishi. Lengo letu ni kuhakikisha usalama na ubora wa huduma zinazotolewa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama na kuongea katika Bunge lako la Kumi na Mbili, nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehma lakini wapiga kura wa Tanga Mjini kwa kunirudisha Bungeni. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini kwamba naweza kumsaidia kusimamia na kuratibu shughuli za utawala na maendeleo katika Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nimpongeze Waziri wa Fedha, ndugu yetu Mheshimiwa Mwigulu kwa kuwasilisha Mapendekezo ya Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano. Katika hatua hii, niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri kwa sababu nimeona Waheshimiwa Wabunge wengi pia wamechangia moja ya vipaumbele vitano vya Mpango wa Taifa wa Maendeleo ambao ni kuchochea maendeleo ya watu. Katika maoni ya Waheshimiwa Wabunge, niseme kwamba tumepokea na ufafanuzi mkubwa au zaidi tutautoa tarehe 19 - 21 wakati tutakapowasilisha bajeti ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niruhusu niguse maeneo makubwa matatu au manne. Eneo ambalo Waheshimiwa Wabunge wameliongelea ni kuboresha miundombinu ya elimu ya msingi na sekondari. Tunakubaliana na nyie kwamba bado tuna uhaba wa vyumba vya madarasa, madawati, maabara za sayansi pamoja na nyumba za walimu katika Halmashauri zetu, katika Majimbo yetu lakini pia ni lazima tukubali kwamba kazi kubwa na nzuri imefanyika katika kipindi cha mwaka uliopita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaeleze tu Waheshimiwa Wabunge kwamba katika bajeti yetu 2021/ 2022, tunatarajia kuendeleza ujenzi wa madarasa ikiwemo kukamilisha maboma ya vyumba vya madarasa 2,695. Pia tutajenga maabara za sayansi takribani 1,280. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha, tumefanya tathmini na hili ni juzi tu, ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais Samia kwamba hataki kuona mtoto wa Kitanzania akisoma chini ya mti akifundishwa katika shule yenye mwalimu mmoja au shule yenye walimu wawili. Kwa hiyo, tumefanya tathmini tuna upungufu wa madawati takribani 1,048,000. Katika bajeti yetu inayokuja tumepanga kununua au kutengeneza madawati 710,000 ili kuweza kutatua changamoto hii ya madawati. Pia tumeona tusiwaache walimu, ni lazima tujenge nyumba za walimu hususani katika maeneo ya pembezoni au maeneo ambayo yapo kidogo mbali na miji mikuu. Kwa hiyo, katika bajeti pia tutajenga nyumba 100 za walimu ili kuhakikisha kwamba tunaweka mazingira mazuri kwa walimu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda naomba nisema kwamba tukijadili bajeti yetu tutaeleza mambo gani makubwa ambayo tutayafanya katika kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia watoto wetu. Kubwa ni commitment ya Serikali kuhakikisha tunatoa elimu bora na sio bora elimu kwa watoto wa kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni watumishi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa na Mikoa ikiwemo changamoto ya uhamisho wa walimu. Katika hili, nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge, kila mtumishi wa Halmashauri anataka kwenda kufanya kazi Halmashauri za Mijini, nani atafanya kazi katika Halmashauri za Vijijini au za pembezoni? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafahamu mwalimu au muuguzi au daktari anayo haki ya kuhama kama mtumishi mwingine wa umma, lakini lazima tuangalie kule vijijini na pembezoni nani anaenda kufanya kazi. Kwa hiyo, hili tumelipokea kwamba Waheshimiwa Wabunge wamelitolea maoni, tutahakikisha kwamba tuna-review case by case lakini tutatoa mwongozo mahsusi kwa ajili ya ku-make sure walimu wanapenda kufanya kazi katika Halmashauri za pembezoni. Kubwa ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na incentive kwa walimu na watumishi wa afya ambao wanafanya kazi katika Halmashauri za pembezoni, kwa hiyo hili tutaliangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni uboreshaji wa huduma za afya ya msingi. Kwenye hili tunapokea maoni na ushauri wa Wabunge kuhusu utolewaji wa huduma. Tunakubaliana na Waheshimiwa Wabunge kwamba bado tuna uhaba wa zahanati, vituo vya afya, pamoja na Hospitali za Halmashauri. Sasa hivi tumeamua kushusha badala ya kuwa Hospitali za Wilaya tunaenda kuwa ni Hospitali za Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kipaumbele chetu cha kwanza katika kuboresha huduma za afya ya msingi, tunaangalia utoaji wa huduma katika ngazi ya zahanati, kituo cha afya pamoja na ngazi ya Hospitali ya Halmashauri. Kwa hiyo haya mambo tarehe 19 mtakuja kuyaona katika bajeti yetu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, nafahamu Wabunge wengi wanataka tujenge zahanati na vituo vya afya, tunaona tujikite kwanza kumaliza zahanati na vituo vya afya ambavyo vimejengwa na havijakamilika. Tumeonyesha katika bajeti yetu tuna vituo vya afya 52 ambavyo tunatakiwa kuvikamilisha lakini pia tuna hospitali za Halmashauri 68 ikiwemo kuhakikisha tunaviwekea vifaa tiba na vifaa pamoja na upatikanaji wa dawa na watumishi ili huduma bora za afya ya msingi ziweze kutolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumepokea ushauri wa kuboresha huduma katika ngazi ya msingi especially huduma za kinga. Hili tumelipokea, ni kweli tukiweza kuzuia wananchi wengi wakawa wana afya bora kabla hawajaenda katika ngazi ya rufaa maana yake pia tutaokoa fedha nyingi za Serikali.

Mheshimiwa Spika, katika suala la afya pia katika bajeti inayokuja Mheshimiwa Rais Samia amenielekeza, haikuwepo kwenye bajeti hii, lakini sasa ametafuta rasilimali fedha, Halmashauri zote 24 ambazo hazina Hospitali za Halmashauri tunaenda kujenga Hospitali za Halmashauri katika Halmashauri hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, muda umeisha lakini nataka kusema suala la TARURA tumelipokea ikiwemo kuongeza bajeti ya TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na mimi naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kuongea katika Bunge hili la Kumi na Mbili kama Waziri wa Afya, niruhusu nianze kumshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuniamini kuendelea kuwa msaidizi wake. Nimwahidi Mheshimiwa Rais, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwamba mimi na Mheshimiwa Dkt. Mollel tutaifanya kazi hii kwa kasi, ubunifu na weledi katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa kila Mtanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze pia kwa kuunga mkono hoja za Kamati zetu mbili; Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii pamoja na Kamati ya UKIMWI. Niishukuru sana Kamati zetu zote mbili na Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri. Tumepokea na niwaahidi kwamba tutafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niseme mambo makubwa matatu. Jambo la kwanza ambalo limeongelewa kwenye Kamati na Waheshimiwa Wabunge ni suala la upatikanaji wa dawa. Katika Bunge hili zamani tunapoongea suala la dawa tulikuwa tunaongea ukosefu wa fedha za dawa, lakini tunamshukuru Rais Samia suala la dawa siyo suala la ukosefu wa fedha za dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kukiri kwamba tunahitaji kujipanga zaidi katika kuhakikisha kwamba dawa zinapatikana, kwa sababu tangu Rais Samia ameingia madarakani tayari Serikali imeshapeleka MSD zaidi ya bilioni 333. Sasa hivi kila mwezi tunapokea bilioni 15 kwa ajili ya dawa, vifaa na vifaatiba.

Kwa hiyo nikiri kweli, maana ukificha maradhi kifo hukuumbua, hali ya upatikanaji wa dawa hairidhishi. Kwa hiyo tunaangalia, tutaendelea kuboresha utendaji wa MSD ili iweze kutekeleza kikamilifu majukumu yake ya ununuzi, utunzaji na usambazaji wa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nilishafika MSD nikawaambia badala ya kupima upatikanaji wa dawa kwa kuwa na dawa za mwezi mmoja tutawapima kwa kuangalia dawa za miezi mitatu. Kuna Mheshimiwa Mbunge amesema dawa zinapelekwa wiki moja zinaisha kwa sababu dawa za miezi mitatu zinapelekwa dawa za siku mbili au tatu. Kwa hiyo hili tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, siyo tu MSD, MSD anaweza aka-procure dawa, lakini upatikanaji wa dawa katika ngazi za vituo vya kutoa huduma za afya kuanzia zahanati hadi hospitali zetu. Kwa hiyo pia tutaimarisha usimamizi wa suala zima la upatikanaji wa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye usimamizi tumeona, na nashukuru Kamati pia imezungumzia suala la ulinganifu wa usambazaji wa dawa kwenye vituo. Kwa hiyo tutafufua zile timu za upembuzi yakinifu wa mahitaji ya dawa kulingana na magonjwa katika eneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, saa nyingine navyo vituo vyetu kila mtu anajua top ten diseases katika eneo lake. Sasa badala ya kufanya quantification ya dawa anazohitaji kwa watu anaowahudumia analeta makisio madogo; kwa hiyo hili pia tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kwa upande wa usimamizi wa dawa, kuna Mwongozo wa Taifa wa Matibabu (Standard National Treatment Guidelines), inasema dawa gani zinatakiwa zitolewe katika level gani. Tumeona, watu wetu badala ya kutoa, sisi kama Serikali tunatumia dawa ambazo ni generic, siyo brand, kwa hiyo unakuta mtu ameandikiwa paracetamol daktari anamuandikia Panadol, Panadol hazipo katika vituo vyetu vya kutoa huduma za afya kwa sababu ile ni brand, sisi tunatumia generic.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dawa ya matibabu ya maambukizi kwa mfano, flagyl, flagyl ni brand, kwa hiyo daktari unapomwandikia mgonjwa flagyl wakati mwongozo unakwambia ni metronidazole, tumeona pia ni tatizo, kwa hiyo tutaimarisha wataalam wetu wazingatie Mwongozo wa Taifa wa Matibabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda unakwenda. Suala la pili ni suala la bima ya afya kwa wotee… kabla ya hili, MSD kuhusu uzalishaji wa ndani wa dawa tunashukuru sheria imepita na tayari Serikali imeshatoa fedha zaidi ya bilioni 15.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.

MWENYEKITI: Nakuongezea dakika moja uzungumzie hilo suala la bima ya afya kwa wote.

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bima ya afya kwa wote, tumepokea maoni na ushauri. Tayari tulishakwenda kwenye Baraza la Mawaziri, tumepokea maelekezo ya Baraza la Mawaziri, tumeyafanyia kazi sasa hivi tuko tayari kurudi tena kwenye Baraza la Mawaziri kwa ajili ya kuomba kupitisha Sheria hiyo ya Bima ya Afya kwa kila Mtu. Kwa sababu tunaamini kwa kweli ndiyo itaweza pia kuwawezesha Watanzania kupata huduma bora za afya bila ya kikwazo cha fedha. Tunaona Watanzania wanauza mashamba yao, wanauza baiskeli pale ambapo wanapata mgonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme tumepokea maoni na ushauri kuhusu non-communicable diseases (magonjwa yasiyo ya kuambukiza), tutawekeza kwenye elimu pamoja na community health workers (wahudumu wa afya ngazi ya jamii) ili waweze kutoa elimu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, tayari ameshaanza kuratibu implementation ya activities mbalimbali katika mapambano dhidi ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza. Kwa hiyo suala hili tayari Waziri Mkuu yupo on-board na analisimamia kwa ukaribu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, tunashukuru kwa maoni na ushauri na tutayafanyia kazi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi. Nami naomba kuchangia hoja hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri jinsi gani tunaweza kuboresha upatikana wa huduma za afya kwa Watanzania, mengi tutayajibu katika mjadala wa bajeti yetu ya Wizara ya Afya na leo niseme jambo moja ambalo lilielezwa kwenye mjadala huu nalo ni kuhusu umuhimu wa Bohari ya Dawa (MSD) kununua dawa kutoka kwa wazalishaji.

Mheshimiwa Spika, Rais wa Awamu ya Tano Mwenyezi Mungu amrehemu uko alipo Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, alipoingia madarakani kati ya jambo moja alilolieleza ni kututaka Wizara ya Afya kupitia MSD kununua dawa moja kwa moja kutoka viwandani au kwa wazalishaji.

Mheshimiwa Spika, tulikuja Bungeni kuleta mapendekezo kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kufanya mabadiliko ya Sheria ya Manunuzi (Procurement Act) mwaka 2016. Kwanza tukafanya kipengele cha kuruhusu manunuzi ya dharura kwa sababu dawa ni bidhaa za kuokoa maisha. Jambo la pili kukaingizwa section 65A ambacho kinasema a procuring entity or the agency shall for the purpose of obtaining value for money in terms of price, quality and delivery. Procure goods or services directly from the manufacturer, dealer, wholesaler or service provider. Kwa hiyo, huu ndiyo msimamo wa sheria.

Mheshimiwa Spika, MSD hazuiwi na sheria kununua moja kwa moja kutoka viwandani au kwa wazalishaji, lengo kushusha gharama ya dawa. Sheria imeweka mipaka siyo tu gharama, quality (ubora) wa dawa, efficacy (ufanisi) wa dawa na upatikanaji wa dawa.

Mheshimiwa Spika, kanuni za manunuzi ya umma kwa sababu suala hili ni nyeti likaweka utaratibu maalum wa kuwezesha manunuzi ya dawa, vifaa na vifaatiba Kanuni ya kuanzia 139 hadi Kanuni ya 147 na inarudia vilevile kwamba tunayo fursa ya kununua moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji, hili nafurahi tulilitekeleza.

Mheshimiwa Spika, 2017 nilipata heshima pia ya kuwa Waziri wa Afya. Tuliingia mikataba 73 na wazalishaji 46 wa dawa kutoka Uganda, Denmark, Ufaransa, Ujerumani, China, Afrika Kusini, Falme za Kiarabu, Bangladesh, India, Kenya na Tanzania. Tuka-identify aina za dawa 178 lakini pia vifaatiba 195 na vitendanishi 178. Kwa hiyo, hili suala siyo geni limeshafanyika. Lengo ni kushusha gharama ya dawa.

Mheshimiwa Spika, nataka nitoe mfano. Baada ya utaratibu huu kuanza kutumika mfano dawa ya chanjo ya homa ya ini, hepatitis ‘B’ vaccine kabla ya kununua viwandani ilikuwa inauzwa elfu 22,000 sasa ikashuka mpaka elfu 5,300. Dawa ya sindano ya diclofenac kwa ajili ya maumivu vichupa 10 ilikuwa inauzwa Shilingi 2,000 ikashuka mpaka 800/= Dawa ya kupambana na maambukizi ya bakteria Amoxicillin miligramu 265 yenye vidonge 15 kwa supplier ilikuwa inauzwa 9,800/= ikashuka mpaka 4,000, mashuka yalikuwa yanauzwa elfu 22,000 yakashuka mpaka elfu 11,100.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili jambo na ndiyo muelekeo wa Wizara Waheshimiwa Wabunge na Serikali kwa ujumla ili kushusha gharama za dawa, dawa zitanunuliwa moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji.

Mheshimiwa Spika, wakati tunatafuta unafuu wa dawa hatuta-compromise ubora wa dawa lakini pia na usalama wa dawa. Tunafahamu hata leo ukienda kariakoo utapata shati la Shilingi 10,000 lakini kuna shati hilo hilo linauzwa Shilingi 30,000. Shati la Shilingi 10,000 linaweza likakaa siku moja la Shilingi 30,000 likadumu hata mwaka mmoja au miaka miwili. Hili ni jambo lazima pia tuli-take into consideration. Kwa hiyo, ninachotaka kumaliza Sheria ya Manunuzi ya Umma haijaweka kikwazo kwa dawa kutonunuliwa moja kwa moja viwandani.

SPIKA: Haya ahsante sana.

WAZIRI WA AFYA: Tunalifanyia kazi lakini ninachotaka kusema...

SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na sisi tutaendelea kuboresha upatikanaji wa dawa salama na zenye ubora. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nami nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma ya Maendeleo ya Jamii inayoongozwa na Mheshimiwa Mbunge Stanslaus Haroon Nyongo kwa maoni na ushauri wao katika kuboresha utoaji wa Huduma za Afya kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli nami nasema kwamba naishukuru sana Kamati, hawakueleza mambo mengi, sana sana mambo ambayo yameibuka katika maazimio ya Kamati au maoni na ushauri wa Kamati ni mambo matano na nitayatolea ufafanuzi kama kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu utengwaji wa bajeti kwa ajili ya kutekeleza shughuli za Wizara na kutekeleza miradi ya maendeleo, tumelipokea, na niseme kwamba Serikali naendelea kutoa fedha nyingi kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli za sekta ya afya na pia kwa miradi ya maendeleo. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ambaye kwa kweli huduma za afya ni moja ya vipaumbele vyake. Kwa hiyo, hili suala tunahakikisha kwamba fedha zitakuja.

Mheshimiwa Spika, pia tuliahidi Bunge lako Tukufu tunapata pia fedha za maendeleo kutoka kwa wadau wa maendeleo, nazo tutazisimamia kikamimilifu kuhakikisha kwamba sambamba na fedha zinazopitishwa na Bunge, lakini pia fedha hizi za wadau wa maendeleo nazo zinatumika kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili ya Kamati ilikuwa ni kuhakikisha kwamba tunaimarisha utendaji wa Taasisi ya Dawa na Vifaa Tiba ili kuzuia uingizwaji wa bidhaa bandia za chakula dawa na vipodozi. Hili nalo tunalipongeza na tumetunga kanuni ambayo inasimamia uingizaji wa dawa katika mipaka 15.

Mheshimiwa Spika, naomba nikiri. Kweli tunayo changamoto kwa sababu ya mipaka yetu isiyo rasmi. Kwa hiyo, tupo katika mipaka rasmi, hivyo ni kweli mipaka ambayo siyo rasmi dawa zinaingizwa na vifaa tiba ambavyo havina ubora. Tumeamua kung’atua madaraka ya TMDA kwa watu ambao ni wataalamu wa dawa katika ngazi za Halmashauri, na wenyewe tumewapa vitambulisho, wanaweza wakafanya pia ukaguzi wa dawa na vifaa tiba katika maduka ambayo yako mitaani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo tumeliona ni kuimarisha utendaji wa Baraza la Wafamasia. Sasa hivi Baraza la Wafamasia wanafanya ukaguzi wa maduka ya dawa na sehemu za kuhifadhi dawa, TMDA naye anafanya. Kwa hiyo, tunataka Baraza la Wafamasia wao wasimamie fani; wataalamu wa famasia, kama Baraza la Madaktari na Baraza la Wauguzi yanavyofanya, halafu tumwachie TMDA mamlaka ya dawa na vifaa tiba kazi ya kukagua premises (maduka ya dawa). Kwa hiyo, Baraza la Famasia akienda kwenye famasi au sehemu yoyote anamwangalia mwanataaluma, siyo suala la dawa, vifaa na vifaa tiba. Tunaamini kwa hatua hii pia itaimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa dawa na vifaa tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo pia limeelezwa na Kamati, na Mheshimiwa Hhayuma ambaye pia ni mtaalamu wa eneo hili, ni kuhakikisha kwamba tunaratibu udhibiti wa chakula na vipodozi ndani ya Serikali. Suala hili lilifika kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, tayari linafanyiwa kazi ndani ya Serikali kati ya TBS na TMDA. Naamini Serikali itafanya maamuzi kuhusu udhibiti na usimamizi wa chakula na vipodozi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli anachokisema Mheshimiwa Hhayuma na Kamati, dawa na vipodozi vinauzwa katika sehehmu moja. Pia sasa hivi tumeona kuibuka kwa supplements, vitamins; sasa regulator siyo tena mtu ambaye anasimamia public health. Kwa hiyo, ni jambo ambalo tumeliona ndani ya Serikali tunaamini kwamba suluhisho litapatikana.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni la MSD (bohari ya dawa). Tunaishukuru sana Kamati, na kipekee kwa kweli tunapongeza maboresho ambayo yameanza kuonekana ndani ya MSD, na Kamati sasa inatushauri tuweke mikakati thabiti ya kushirikisha sekta binafsi katika uwekezaji wa Viwanda vya Dawa na Vifaa tiba vinavyozalishwa ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, jambo hili tunalikubali. Nami nilishawaelekeza MSD, as long as dawa au kifaa tiba kinazalishwa na kiwanda cha ndani chenye ubora na bei; na bei tumesema kama dawa hiyo au kifaa tiba hicho kinazalishwa na kiwanda cha ndani cha Tanzania, bei yake imezidi kwa asilimia 15 wanunue bidhaa hiyo ambayo inazalishwa ndani ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka kutoa mfano. Tumeanza kununua IV fluids kutoka Kairuki Pharmaceticals badala ya kununua kutoka Uganda. Nitoe rai kwa wazalishaji wa ndani wa dawa na vifaa tiba. Naogopa isije kutokea tukapiga marufuku tusinunue kutoka nje ya nchi, lakini labda hawana uwezo au capacity ya kukidhi mahitaji ya dawa na vifaa tiba ya ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, nilikutana nao mwezi Januari, tumekubaliana. Kwa hiyo, tutafanya tathmini; huyu uwezo wake ni kuzalisha dawa zipi na kiasi gani? Tukishajua tumeshamwelekeza MSD, marufuku kuleta dawa kutoka nje ya nchi kama dawa hiyo inapatikana ndani ya nchi na ina ubora na pamoja na suala la gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wazalishaji wa ndani wa viwanda vya dawa pia wametuambia, tukinunua nje ya nchi, tunawapa Letter of Credit, ndani ya nchi hatuwapi chochote. Kwa hiyo, suala hili tayari nimemwomba Waziri wa Fedha, tutakutana nao. Hata kama hatutawapa Letter of Credit, lakini tuangalie kama tunaweza tukawapa advance amount ili waweze sasa kujipanga vizuri kununua raw material ili waweze kuzalisha dawa na vifaa tiba ambavyo vinahitajika ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo limeelezwa na Kamati ni kuimarisha tafiti za ubora athari na matumizi salama ya tiba asili chini ya NIMR, Medical Research Institute, Taasisi ya Magonjwa ya Binadamu. Tunapokea ushauri wa Kamati, tutalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunaona ni kweli, kuna ujanja ujanja. Utaambiwa dawa hii inatibu saratani, dawa hii inatibu kisukari, dawa hii inatibu magonjwa ya moyo, lakini ukiangalia ufanisi (efficacy) wake, tumeona Watanzania pia wanaibiwa. Ila kwa kweli tunakubali kwamba wapo Watanzania ambao wanatengeneza tiba asili ambazo zingeweza kusaidia na kuokoa maisha ya wengi. Kwa hiyo, tutaongeza fedha za ndani kwa NIMR kama kamati ilivyo tushauri ili weweze kufanya utafiti.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo limeelezwa na kaka yangu Mheshimiwa Kakunda, nimelipokea kuhusu michoro ya vituo vya kutoa huduma za afya, tutaliangalia. Naomba nitahadharishe, tujengeni miundombinu ya kutoa huduma za afya kwa kuangalia mahitaji ya sasa na mahitaji ya miaka 20, 30 inayokuja. Maana sasa hivi jinsi unavyoboresha huduma, ndivyo wananchi wanavyodai huduma bora zaidi, ndivyo wananchi wanavyodai huduma za ngazi ya juu zaidi kuliko zahanati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nakubaliana na kaka yangu Mheshimiwa Kakunda katika suala la gharama, lakini gharama hii itakidhi mahitaji ya sasa ya kutoa huduma za afya kwa kizazi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: dakika moja Mheshimiwa Waziri umalizie.

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mheshimiwa Kakunda tumepokea ushauri wako, tutaufanyia kazi, tutatoa michoro kwa kushirikiana na TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, naomba nimalize kwa kukushukuru sana lakini kuishukuru Kamati yetu ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, wanafanya kazi kubwa na nzuri sana ya kutushauri, nasi tunawaahidi kwamba tutaboresha utoaji wa huduma za afya especially tunapoelekea kwenye Bima ya Afya kwa wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii. Vile vile nakupongeza kwa kuongoza vema Bunge letu. Pili, nawapongeza sana Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati zote tatu, PAC, LAAC na PIC kwa taarifa zao nzuri ambazo sisi kama Sekta ya Afya kupitia Wizara ya Afya tunazipokea na mapendekezo yao yote tunayapokea na tunawaahidi kwamba tutayafanyia kazi. Kipekee nampongeza sana CAG kwa kufanya kazi yake ya kikatiba ya kudhibiti na kukagua fedha za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee tunataka kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge wote kwamba kila senti inayotolewa na Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa ajili ya kuboresha huduma za afya tutaisimamia kikamilifu. Katika kipindi cha miaka miwili tunamshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Sekta ya Afya tumepokea shilingi trilioni 6.7, haijapata kutokea katika historia ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, niruhusu sasa nijielekeze kwenye hoja kama tatu ambazo zimeletwa kwenye Bunge lako tukufu. Kamati ya PAC, PIC na LAAC, walileta hoja kuhusu MSD. Suala la kwanza la MSD ni suala la ukiukwaji wa sheria katika ununuzi wa vifaatiba kutoka kampuni ya Misri ya Alhandasya, shilingi bilioni 3.4. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, tunazingatia sheria, kanuni na taratibu. Sisi kama Serikali tumeanza kuchukua hatua za kiutawala ambapo Mtendaji Mkuu wa MSD tulimwondoa tarehe 12 Aprili, 2022. Hatukuishia hapo, tumeondoa Wakurugenzi sita wote wa MSD, Mkurugenzi wa Fedha na Mipango, Mkurugenzi wa Ununuzi, Mkurugenzi wa Utawala, Mkurugenzi wa Usambaaji wa Huduma za Kanda, Meneja wa Sheria na Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa MSD. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, unaweza ukaona dhamira ya dhati ya Serikali katika kuwashughulikia watu wanaotuhumiwa kutenda ubadhirifu katika fedha za Umma. Kama haitoshi…

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ummy Mwalimu, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Anatropia.

TAARIFA

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa mchango anaoendelea nao, amekiri kwamba kulikuwa na ukiukwaji wa taratibu na waliohusika waliondolewa. Moja kati ya kilio cha Wabunge na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, ni watu kuondolewa kutoka kwenye eneo moja kwenda eneo lingine. Aliyekuwa sasa Msimamizi ambaye alikuwa Mwanajeshi, ameondolea amepelekwa Jeshini. Yuko hai, alihusika katika hiii mikataba na fedha kupotea. Tunataka sasa tujue ni hatua gani zilichukuliwa, pamoja na kumkamata yeye ili tusaidie kurudisha hichi kiasi? (Makofi)

SPIKA: Haya, ahsante sana. Mheshimiwa, Ummy Mwalimu.

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, tumeapa mbele ya Bunge lako tukufu kulinda Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, lazima tufuate Sheria na Kanuni za Kiserikali. Mheshimiwa Simbachawene, ameeleza vizuri, vyombo vyenye mamlaka ya kufanya uchunguzi wanaendelea na kazi. Kwa sababu, sheria yetu inazungumzia presumption of innocent, ndiyo maana tumechukua maamuzi ya kiutawala, tuache vyombo vifanye kazi yao ya taratibu nyingine za kijinai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kuwahakikishia, hatukuishia tu kwenye Wakurugenzi sita wa MSD, tumebadilisha Mameneja wa Kanda wote nane wa MSD. Kwanza, sisi Wizara ya Afya hatukusubiri hata Taarifa ya CAG. Tulifanya special audit wenyewe, tukaleta humu na baadhi yetu sisi tulituhumiwa na baadhi ya Wabunge kwamba sisi tunawaweka pembeni baadhi yao, lakini tulikuwa tunajua tunachokifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba niseme, kila senti ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan inayopelekwa kwenye Sekta ya Afya tutaisimamia. Nitume salamu kwa watendaji wote wa MSD na wengine katika Sekta ya Afya, hatutawavumilia. Tutachukua hatua mara moja ili kulinda fedha za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo kwa sababu ya muda ni suala ya Bohari ya Dawa. Hii ni hoja ya LAAC kutopeleka dawa na vifaa tiba shilingi bilioni 8.6.

Mheshimiwa Spika, suala hili tayari tumeshalifanyia kazi, kwa mfano Halmashauri ya Mbinga walikuwa wanadai milioni 577 vifaa tiba wamepokea vifaa tiba vya milioni 846. Maswa walikuwa wanadai milioni 558 wameshapelekewa bidhaa za milioni 810. Pia Dar es Saalam walikuwa wanadai bilioni 2.9 wamepelekewa vifaa vyenye thamani ya bilioni 2.8.

Mheshimiwa Spika, kubwa ambalo nataka kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, yapo mabadiliko makubwa ndani ya MSD. Tukiangalia thamani ya bidhaa zilizosambazwa na MSD mwaka wa fedha 2021/2022 wamesambaza vifaa vyenye thamani ya bilioni 315, mwaka 2023 375 kwa hiyo ongezeko la bilioni 58. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaangalia pia mapato revenue. Mwaka jana quarter ya kwanza MSD alipata mapato ya bilioni 77.9 quarter ya 2024 MSD imepata mapato ya bilioni 113. Hii inaonyesha maoni na ushauri wa Wabunge tumeufanyia kazi na niwaambie Waheshimiwa Wabunge tutaendelea kufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala la MSD kupokea dawa ambazo zinakaribia kuisha muda limeletwa na Kamati ya PIC ni kweeli mwongozo ambao unatutaka tupokee bidhaa za dawa zinatakiwa zisiwe chini ya miezi 28 au 80% lakini pia kama Wanasheria wanavyojua kwenye general rule lazima kuwe na exceptions kwa hiyo, ipo sheria inayoturuhusu.

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya bidhaa mnaweza mkazipokea chini ya wiki, chini ya shelf life ya wiki 24 pale ambapo bidhaa hiyo inaweza kutumika kwa ajili ya kutibu magonjwa mahususi. Kuna vitu vitendanishi vinaitwa control, hivyo vinazalishwa ndani ya miezi mitatu kwa hiyo miezi sita ni lazima pia uvipokee chini ya muda huo.

Mheshimiwa Spika, naenda haraka haraka suala la Njombe kwamba MSD alinunua mashine ya bilioni 6.3 haijafungwa. Zipo changamoto tunaendela kuzifanyia kazi lakini pia lazima tuongozwe na Taarifa za Kitaalamu. Jambo hili naomba niseme Kamati ya PAC tumelipokea na tutakuja kuleta ufafanuzi zaidi juu ya suala hili.

Mheshimiwa Spika, nimalize suala la PAC kuhusu NHIF. Hili ni suala la madeni kwamba NHIF wanaidai Serikali bilioni 228. Waheshimiwa Wabunge tumemsikia Waziri wa Fedha katika budget speech hapa wamehaidi kwamba wataanza kurejesha deni hili Wizara ya Mambo ya Ndani bilioni 45, Taasisi ya Mifupa MOI bilioni 18.2 NIDA bilioni 17.3 na Hospitali ya Benjamini Mkapa bilioni 129 wenzetu Wizara ya Fedha tayari wameshalihakiki deni hili na wameahidi kulilipa ili kulinda uhai na uendelevu wa NHIF. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kengele ya pili ilishagonga.

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Wakala wa Kimataifa wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu (International Renewable Energy Agency - IRENA) na Azimio la Bunge kuhusu mapendekezo ya kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika wa Mwaka 2019 (Treaty for the Establishment of the African Medicine Agency - AMA)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru wachangiaji wote ambao wamechangia hoja yangu ya kuomba Bunge lako lipitishe Azimio kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli maoni yote ambayo yametolewa yanaunga mkono Azimio. Niseme kubwa, sisi kama Serikali tunaamini kwamba kuridhiwa kwa mkataba huu wa AMA, itakuwa ni moja ya nyenzo muhimu katika kupambana na bidhaa tiba duni na bandia, kukuza soko la bidhaa tiba ambazo zinaweza kuzalishwa na nchi nyingine. Kwa hiyo, kubwa tunaamini tutanufaika zaidi na Azimio hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati imeunga mkono jambo kubwa ambalo Kamati imesema na Mheshimiwa Christina Mnzava, ni kwa nini tumechelewa? Ndiyo taratibu zetu za Serikali, lakini naamini maazimio mengine ambayo yana maslahi makubwa kwa nchi tutajitahidi kuyaleta kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Askofu Josephat Gwajima kwa kweli ameongea jambo kubwa sana zuri na inaonekana amefanya research kwenye masuala ya teknolojia ya genetics. Ni kweli ndiyo tiba sasa hivi, hata kwenye masuala ya stem cell therapy, masuala sasa hivi ndiyo yanajitokeza. Kwa hiyo, Azimio hili pia linakwenda kudhibiti, maana sasa hivi hatuna sheria ya kudhibiti masuala kama hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kusema kama walivyosema Dkt. Ndugulile, Askofu Gwajima na Mheshimiwa Christina Mnzava na Kamati ya Mheshimiwa Nyongo. Kweli dawa ni maisha, biashara na siasa. kwenye biashara ukiangalia baada ya biashara haramu ya silaha, dawa za kulevya, dawa ni moja pia ya biashara tatu kubwa ambazo zina-generate mapato makubwa sana. Kwa hiyo ni lazima pia tuimarishe mifumo na uwezo wa nchi katika kudhibiti dawa, vifaa tiba vitendanishi pamoja na bidhaa nyingine za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, angalizo ambalo limetolewa na Mheshimiwa Dkt. Ndugulile tumelipokea, kuhusu masuala ya udhibiti wa chakula tutaendelea kujadiliana ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, angalizo lingine ambalo tunaenda nalo ni kuimarisha uzalishaji wa ndani wa dawa. Sasa hivi kwa mfano katika maji tiba (drip) tunavyo viwanda viwili ambayo vinazalisha Maji tiba na kukidhi soko la nchi. Tunayo Kairuki Pharmaceuticals na Alfa Pharmaceuticals, wana uwezo wa kuzalisha chupa 98,000,000 za maji tiba wakati mahitaji ya nchi ni chupa 24,000,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunaamini kabisa tukipitisha Azimio hili pia as long as nchi nyingine zimeridhia Mkataba wa AMA tuna uwezo wa kwenda kuuza ziada katika chi nyingine za Afrika. Pia kubwa tumepata maoni kuna wawekezaji wako tayari kuja nchini, lakini wananiambia Minister, when we come to Tanzania, we can’t sell for Tanzanian market. We have also to sell for SADC and EAC. What are the requirements? Kwamba, do we need also to register our products in Kenya, Rwanda, Burundi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tukipitisha mkataba huu na kama Kenya ameridhia, Zambia, Rwanda, Burundi, Zimbabwe, maana yake wawekezaji pia watavutika kuja kuwekeza Tanzania na hivyo bidhaa zao kuuzwa katika nchi nyingine za Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, kama Serikali tutaendelea kutoa kipaumbele kwa bidhaa za afya, bidhaa tiba zinazozalishwa ndani ya nchi. Mwaka jana tulinunua bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi zenye thamani ya shilingi 14,000,000,000. Mwaka 2023 tumenunua bidhaa za afya zinazozalishwa ndani ya nchi zenye thamani ya shilingi 36,000,000,000. Kutoka shilingi 14,000,000,000 mpaka shilingi 36,000,000,000. Kwa hiyo naiona commitment ya Serikali katika kuimarisha uzalishaji wa ndani wa bidhaa tiba. Tunaamini kabisa mkataba huu pia utatuwezesha kufikia lengo la Serikali la kupunguza uagizaji bidhaa tiba kutoka nje ya nchi angalau kwa 50% ifikapo mwaka 2030.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa Bunge lako lipitishe Azimio kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika (Treaty for the Establishment of the African Medicines Agency - AMA).

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 7) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na timu yake kwa maandalizi mazuri ya Muswada huu wa Sheria mbalimbali. Pili, nimshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria, Wakili msomi Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa pamoja na Wajumbe ambao wameutendea haki Muswada huu ambao uko mbele ya Bunge lako tukufu. Namshukuru pia Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwa taarifa yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda, jambo la kwanza muhimu, lengo la Serikali kuleta mapendekezo ya Marekebisho ya Sheria ya Udhibiti wa UKIMWI. Kubwa ni kutaka kuongeza kasi ya kuweza kufikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030, na hili linawezekana. Kwa hiyo tumejiwekea malengo mpaka mwaka 2020, tuwe angalau tumefikia zile 90 tatu. Kwa hiyo 90 ya pili tunafanya vizuri, watu ambao wanatumia ARV na 90 ya tatu tunafanya vizuri kwa wale watu ambao wanatumia ARV kwamba, kiwango cha Virus vya UKIMWI kimeweza kupungua (Viral load suppression). Kwa hiyo, changamoto iko kwenye 90 ya kwanza, tuko kwenye asilimia 62, kwa hiyo tumeona kama Serikali tuje na mikakati mbalimbali ambayo itasukuma watanzania kupima UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja kubwa ambayo inabishaniwa, ambayo imeletwa labda na wenzetu wa Kambi ya Upinzani ni kushusha umri wa mtoto kujipima bila ridhaa ya wazazi hadi miaka 12. Kwanza kubwa, mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 15 hakatazwi kupima lakini kama anataka kupima, bado msimamo wa Serikali apime kwa ridhaa ya wazazi au walezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusitake tu kuiga mambo ambayo yanatokea, na tunao ushahidi wa nchi za SADC, hali ikoje. Kwa hiyo, ndiyo maana tumekuja, ilikuwa miaka 18, tumepima, hebu tushushe mpaka miaka 15 na tunazo takwimu zinaongea. Maambukizi ya UKIMWI kwa watu wa umri wa chini ya miaka 14 ni 0.04%, sasa hawa unasema wakajipime bila ridhaa ya wazazi. Na tukiangalia ni mother to child transmission, wengi wamepata haya maambukizi. Kwa hiyo, bado ni msimamo wa Serikali, pale ambapo mtu ana umri wa chini ya miaka 15 na anataka kupima, basi atapima pale ambapo kuna ridhaa ya wazazi au walezi. Kama wa miaka 15 ndiyo tunamruhusu kujipima na amesema Mheshimiwa Mwakasaka, umenisaidia sana. Ametoa hoja South Afrika wameshuka mpaka 12 years, maambukizi yametoka 12 percent yameenda 20.4 percent, Lesotho pia yalikuwa 31 very insignificant. Rwanda wao ni 15 years, hawajashusha siyo 12 years.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa sababu ya muda, lakini pia takwimu TDHS (Tanzania Demographic and Health Survey) ya 2015/2016 inaonesha mihemuko ya kufanya mapenzi (ngono) inaanzia miaka 15 siyo chini. Tunazo takwimu hapa, I mean tukiangalia mabadiliko ya kibaiolojia yanaonesha kwamba kwanye TDHS 2015/2016 age of first sexual intercourse, inaonesha ni 43% kwa 15 – 24 years. Hao watoto wanachohitaji ni kuwapa elimu ya kujikinga na Virus vya UKIMWI, elimu kuhusu afya ya uzazi, my body, my protection, elimu ya kujikinga na ubakaji, ulawiti lakini tusiwaingize watoto hawa kwamba waende moja kwa moja kujipima bila mzazi kujua. Halafu akishajipima mzazi hajui anafanyaje! Anaenda kunywa dawa kimya bila mzazi kujua!

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona nisisitize hilo. Jambo la pili ambalo nataka kusisitiza, upo utaratibu kama nilivyosema wa kutoa huduma za upimaji wa Virus vya UKIMWI kwa watoto wa chini ya miaka 15. Kwa hiyo, nimalize tumeshusha umri miaka 18 – 15, tutafanya utekelezaji, baada ya muda hii sheria siyo biblia wala si msaafu, tutakuja kuona hali halisi. Tutafanya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri ahsante, umeieleza vizuri sana na yule ambaye alikwa haelewi sasa ameelewa.