Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Ummy Ally Mwalimu (26 total)

MHE. SUSAN A. J. LYIMO aliuliza:-
Ugonjwa wa kipindupindu umeendelea kukatisha maisha ya watu wengi, japokuwa chanzo chake ni uchafu ambao ungeweza kuzuilika:-
Je, Serikali ina mikakati gani ya kuhakikisha ugonjwa huu unatokomezwa nchini?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susan Anselm Lyimo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu ulianza nchini tarehe 15 Agosti, 2015 katika Mkoa wa Dar es Salaam na baadaye kusambaa katika mikoa mingine ya Tanzania Bara.
Hadi kufikia tarehe 31 Januari, 2016, jumla ya watu 15,067 walikwishaugua ugonjwa huu na kati yao jumla ya watu 233 walifariki dunia. Mikoa ambayo haijaathirika na ugonjwa huu ni Njombe, Ruvuma na Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika kudhibiti ugonjwa huu imeweka mikakati ifuatayo:-
(i) Kuunda Kamati za Kudhibitii Ugonjwa wa Kipindupindu katika ngazi zote;
(ii) Kuelimisha jamii kupitia njia mbalimbali ambazo ni pamoja na mabango, vipeperushi, redio na televisheni; na
(iii) Kuimarisha usafi wa mazingira na usalama wa maji na chakula kwa kufanya yafuatayo:-
(a) Ukaguzi wa vyanzo vya maji katika mikoa iliyoathirika na kufunga vyanzo vya maji vilivyobainika kuwa na vimelea vya kipindupindu na pia kuweka njia mbadala ya kupata maji;
(b) Kutibu maji katika ngazi ya kaya na kufanya ufuatiliaji wa wagonjwa kwenye maeneo yaliyoathiriwa na ugonjwa huu;
(c) Kusambaza dawa ya kutakasa maji ya kunywa (water guard) katika maeneo mbalimbali nchini;
(d) Kushirikikiana na Mikoa na Halmashauri za Wilaya kufanya ukaguzi wa baba au mama lishe na waliokiuka walipewa faini; na
(e) Kunyunyizia dawa ya kuua vAimelea vya ugonjwa wa kipindupindu kwenye vyoo.
MHE. MARIAM N. KISANGI (K.n.y. MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE) aliuliza:-
Hivi karibuni Jimbo la Kigamboni limetangzwa kuwa Wilaya Mpya, hata hivyo wananchi wake bado wanapata huduma ya Mahakama kupitia Wilaya ya Temeke:-
(a) Je, Serikali itaanzisha lini Mahakama ya Wilaya ya Kigamboni?
(b) Je, utekelezaji wa hatua hiyo utaanza lini?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Sheria ya Mahakama ya mwaka 1984, Sura ya 11, inaeleza kwamba baada ya kuanzishwa kwa Wilaya Mpya na kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali uanzishwaji wa Mahakama ya Wilaya inabidi ufanyike. Hivyo, kutokana na Mheshimiwa Rais kuridhia kuanzishwa kwa Wilaya Mpya ya Kigamboni, Mahakama imeweka lengo la kujenga Mahakama ya Wilaya ya Kigamboni kwa kadri fedha za miradi ya maendeleo zitakavyopatikana.
Mheshimiwa Spika, pamoja na kuanzishwa kwa Wilaya, Serikali inaendelea na mpango wa kuboresha majengo na miundombinu ya Mahakama zilizopo Kigamboni. Kwa sasa ujenzi wa jengo jipya la Mahakama kwenye eneo la Mahakama ya Mwanzo Kigamboni unaendelea na unatarajiwa kukamilika mapema Aprili, 2016. Jengo hilo jipya litakuwa na ukubwa wa kutosha na hivyo litakidhi uwepo wa Mahakama ya Mwanzo na ya Wilaya kwa kuanzia.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE (K.n.y. MHE. JOSEPH O. MBILINYI) aliuliza:-
Je, ni lini jengo la maabara ya mionzi linalojengwa kwa muda mrefu sasa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mbeya litakamilika na vipimo vya CT-Scan na MRI-Scan vitaletwa na kuanza kazi?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, niruhusu nitumie Bunge lako Tukufu kuwatakia kheri watoto wote wa Tanzania, watoto wote wa Afrika kwa kuwa leo ni siku ya Mtoto wa Afrika. Kaulimbiu ya mwaka huu tunasema „Ubakaji na Ulawiti kwa Watoto Vinaepukika, Chukua Hatua Kuwalinda Watoto‟.
Mheshimiwa Naibu Spika, Nataka kuwathibitishia watoto wa Tanzania kwamba Serikali ya Awamu ya Tano itahakikisha wabakaji na walawiti wa watoto wanafikiwa na mkono wa dola na kila mbakaji ajiandae kutumikia kifungo cha miaka 30. Tutawalinda watoto wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, nitumie Bunge lako Tukufu kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuwahamasisha wazazi, walezi, kuongeza jitihada za kuwalinda watoto wetu kwa sababu 48% ya ubakaji na ulawiti unatokea katika nyumba zetu. Kwa hiyo, nyumba zetu siyo salama kwa watoto wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, sasa napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Afya ilianza mradi wa ujenzi wa jengo…
NAIBU SPIKA: Mbeya Mjini, Mheshimiwa Waziri.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Osmund Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ilianza mradi wa ujenzi wa Jengo la X-Ray katika Hospitali ya Rufaa Mbeya tarehe 9 Novemba, 2010 lengo likiwa ni kuboresha huduma za uchunguzi katika hospitali hii inayohudumia wakazi wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini. Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2013/2014 hadi 2014/2015 kiasi cha Sh.614,670,000/= kilitolewa kwa ajili ya kuendeleza ujenzi katika mradi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2015/2016 kiasi cha shilingi bilioni 8 kilitengwa, fedha ambayo mpaka sasa haijatolewa. Hata hivyo, Wizara bado ina nia ya kukamilisha ujenzi wa mradi huu, hivyo katika mwaka wa fedha 2016/2017 Wizara imetenga kiasi cha shilingi bilioni 5 katika bajeti ya maendeleo ambazo zitatumika kama ifuatavyo:-
(i) Shilingi bilioni 3 zitatumika kuendeleza ujenzi pamoja na kulipa deni lililobaki kwa mkandarasi aliyekuwa anajenga; na
(ii) Shilingi bilioni 2 zitatumika kununua vifaa tiba zikiwemo CT-Scan na MRI.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni matarajio yangu kwamba ujenzi huu utakamilika mwaka ujao wa fedha 2016/2017 pamoja na kusimika vifaa.
MHE. RITTA E. KABATI (K.n.y. MHE. MGENI JADI KADIKA) aliuliza:-
Tatizo la fistula limekuwa likiwakumba wanawake wengi sana hapa nchini hususan maeneo ya vijijini hali inayowasababishia kuathirika kiakili na kimwili:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kutokomeza tatizo hili hapa nchini?
(b) Kwa sasa ni hospitali moja tu ya CCBRT hapa nchini inayotoa matibabu ya tatizo na iko Dar es Salaam tu; je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka huduma hii katika mikoa mbalimbali au kanda ili wanawake wengi waweze kupata huduma hiyo?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la fistula linatokana na Mwanamke mjamzito kupata uchungu pingamizi kwa muda mrefu. Tatizo hili linaweza kuepukwa iwapo tutakuwa na huduma bora kwa wajawazito ili kuepuka uchungu pingamizi wa muda mrefu. Ili kuboresha huduma kwa wajawazito, Wizara imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwemo kuelimisha jamii kupitia wahudumu wa afya katika jamii na vyombo vya habari kuhusu umuhimu wa kujifungulia katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Pili, kupandisha hadhi baadhi ya vituo vya afya ili viweze kufanya upasuaji wa kumtoa mtoto.
Tatu kuwajengea uwezo watoa huduma ya afya ili waweze kumfuatilia mjamzito wakati wa uchungu wa uzazi na ikibidi aingilie kati kabla kufikia uchungu pingamizi na pia kuboresha mfumo wa rufaa ikiwemo magari ya kubebea wagonjwa.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, huduma kwa wagonjwa wa fistula inatolewa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Hospitali za Rufaa za Kanda za Bugando - Mwanza; KCMC -Moshi; na Mbeya Rufaa. Hospitali nyingine ni pamoja na CCBRT - Dar es Salaam; Peramiho - Ruvuma; Seliani - Arusha; na St. Gasper - Itigi. Jitihada zinaendelea kuwezesha Hospitali za Rufaa za Mikoa ziweze kutoa huduma ya matibabu ya fistula.
MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza:-
Baadhi ya nchi za Afrika kama Uganda na Zimbabwe zimejenga viwanda vyao kwa ajili ya kutengeneza dawa za kupunguza makali ya VVU (Generic za HIV) na hivyo kupunguza gharama za kusaidiwa dawa hizo ambazo zinabadilishwa kila baada ya miaka kadhaa na hivyo
kutengeneza usugu kwa baadhi ya magonjwa.
(a) Je, Serikali ina mpango wowote wa kujenga kiwanda cha kutengeneza ARVs za watu wazima pamoja na watoto?
(b) Kwa dawa zinazoletwa hapa nchini, je, kuna ARVs za watoto?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, kama
ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inahamasisha mashirika, taasisi, wafanyabiashara wakubwa na wawekezaji kuwekeza kwenye viwanda vya kuzalisha dawa mbalimbali zikiwemo dawa za kupunguza makali ya UKIMWI (ARVs).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa kuna kiwanda kimoja Mkoani Arusha TPI ARV Limited ambacho kimepewa leseni ya kutengeneza ARVs. Kiwanda hicho bado hakijaanza uzalishaji. Wizara inatarajia kuwa kiwanda hicho kitaanza uzalishaji wa ARVs hivi karibuni.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu dawa za ARV zinazoingizwa nchini, kuna dawa za watoto ambazo ni pamoja na Nevirapine Syrup, Lopinavir/Ritonavir Syrup, dawa nyingine ni pamoja na mchanganyiko wa dawa za vidonge mfano Lamivudine/Atazanavir zenye nguvu ya miligaramu 30 na miligramu 60 pamoja na Lamivudine zenye nguvu ya miligramu 30 na miligramu 60.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na wananchi wote kwa ujumla kwamba nchi yetu haina tatizo la upungufu wa dawa za ARV kwa watoto.
MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-
Kumekuwa na ongezeko kubwa la watoto wa mitaani hasa katika Miji Mikuu ya nchi yetu.
Je, Serikali inachukua hatua gani kupunguza tatizo hilo ili watoto hao walelewe katika mazingira salama na maadili halisi ya Kitanzania?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa sana, kaka yangu Khatib Said Haji, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa kumekuwa na ongezeko la watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani hasa katika miji mikubwa. Kwa mujibu wa takwimu zilizofanyika katika Majiji ya Dar es Salaam na Mwanza mwaka 2012 zilionesha kuwa Jiji la Dar es Salaam lilikuwa na watoto 5,600 kutoka mikoa kumi ya Tanzania ambayo ni Dar es Salaam yenyewe 28%, Dodoma 9%, Mwanza 7%, Morogoro 7%, Tanga
6%, Lindi 6%, Iringa 5%, Pwani 5%, Kilimanjaro 5% na Arusha 4%.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inalo jukumu la msingi kuhakikisha ulinzi na usalama wa mtoto. Katika kutekeleza wajibu huu, Serikali kwa kushirikiana na wadau, inatekeleza mikakati mbalimbali ikiwemo kuwezesha jamii kuwa na mipango shirikishi ya kuwahudumia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi wakiwemo watoto wa mitaani. Hadi sasa mpango huu unatekelezwa katika Halmashauri 111 nchini.
Aidha, Wizara kwa kushirikiana na TAMISEMI imeanzisha mpango wa kuimarisha ulinzi na usalama kwa watoto ambapo Halmashauri 51 zimewezeshwa kuunda timu za ulinzi wa watoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kueneza mpango huu katika Halmashauri nyingine nchini.
MHE. MGENI JADI KADIKA aliuliza:-
Vijana wengi walioathirika na dawa za kulevya wanaleta kero kubwa ndani ya jamii, kutengwa na wazazi wao na kukosa msaada wa kifedha pale wanapoamua kuacha na kujiunga na kituo cha tiba.
Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa matibabu bure kwa vijana hao ili warudi katika hali zao za kawaida na hatimaye kuendelea na ujenzi wa Taifa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kuwa nchi yetu imeendelea kuwa na wimbi kubwa la ongezeko la matumizi ya dawa za kulevya katika sehemu mbalimbali hapa Tanzania, na hii hupunguza nguvu kazi ya Taifa na kudidimiza uchumi wa nchi yetu. Matumizi ya dawa za kulevya hasa kwa vijana yanaongezeka hapa nchini hasa katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Tanga, Arusha, Mwanza na Mbeya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto imeendelea kutoa huduma kwa waathirika wa matumizi ya dawa za kulevya hapa nchini bila malipo katika vituo mbalimbali vya umma vinavyotoa huduma hizo. Hivi karibuni Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imefungua vituo katika Hospitali ya Muhimbili, Mwananyamala na Temeke kwa Mkoa wa Dar es Salaam ambavyo vimeshahudumia waathirika takribani 3,000 kwa kuwapa tiba ya methadone.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kuongezeka kwa matumizi ya dawa za kulevya, Wizara kwa kushirikiana na Serikali ya Marekani ilianza Mradi wa Utafiti wa Matumizi ya Dawa ya Methadone Hospitali ya Taifa Muhimbili mwaka 2011, na kuonyesha mafanikio makubwa na kufuatia kufunguliwa kwa vituo vya kutolea huduma za methodone katika Hospitali za Rufaa za Temeke na Mwananyamala. Upanuzi wa huduma hizi unaendelea kwa mikoa ya Mwanza na Mbeya ambayo itaanza kutoa huduma hizo hivi karibuni na mikoa mingine itafuata. Arusha, Tanga na Pwani wako katika hatua za awali za kuanza kutoa huduma hizo.
MHE. JORAM I. HONGOLI aliuliza:-
Dawa zinazotolewa na MSD zimekuwa zikichelewa sana kupelekwa kwenye Halmashauri na hivyo kusababisha baadhi ya dawa kupelekwa zikiwa zimekaribia kuisha muda wake wa matumizi hali inayozisababishia Halmashauri gharama kubwa za utekelezaji.
Je, ni kwa nini gharama za uteketezaji wa dawa hizo zigharamiwe na Halmashauri badala ya MSD ambayo inachelewa kuzipeleka?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joram Ismail Hongoli, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, upo utaratibu wa usambazaji wa moja kwa moja wa dawa kwenda kwenye vituo vya kutolea huduma za afya vya umma (direct delivery) unaofanywa na Bohari ya Dawa (MSD). Kwa mujibu wa utaratibu huu, Kamati za Afya za vituo husika hupokea na kuhakiki kila dawa iliyopokelewa kituoni hapo kama inavyoonyeshwa kwenye hati ya madai. Hati hiyo huonyesha gharama za dawa pamoja na muda wa dawa kuisha matumizi yake.
Mheshimiwa Spika, endapo Kamati ya afya ya kituo haitaridhika na kupokea dawa kwa sababu yeyote ile muhimu ikiwa ni pamoja na kuharibika au dawa kuwa na muda mfupi kwa matumizi, kituo hutakiwa kujaza fomu namba saba ili kurudisha bidhaa iliyokataliwa moja kwa moja Bohari ya Dawa ambapo gharama ya dawa husika hurejeshwa kwenye akaunti ya kituo husika.
Mheshimiwa Spika, taarifa za usambazaji wa dawa na vifaa tiba kutoka MSD katika Halmashauri ya Njombe kwa mwaka 2016/2017 hazionyeshi uwepo wa dawa zilizosambazwa zikiwa na muda mfupi wa matumizi. Hivyo, MSD haipaswi kugharamia uteketezaji wa dawa zilizokwisha muda wa matumizi katika Halmashauri ya Njombe kwa kuwa jukumu la uteketezaji ni la Halmashauri husika.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, nitumie Bunge lako Tukufu kuzitaka Halmashauri zote nchini kuzingatia vyema taratibu za kupokea, kuhifadhi na matumizi ya dawa.
MHE. MUSSA B. MBAROUK aliuliza:-
Tafiti zinaonesha Watoto njiti Tanzania wanapoteza maisha wakiwa chini ya miaka mitano:-
(i) Je, Serikali inachukua hatua gani mahsusi kupambana na tatizo hili na kuhakikisha Watoto njiti walio hai wanakua bila matatizo?
(ii) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa elimu kwa Watanzania juu ya sababu zinazosababisha watoto kuzaliwa njiti?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, takwimu zinaonesha kuwa nchini Tanzania asilimia 17 ya watoto huzaliwa kabla ya muda wa mimba kukomaa. Watoto hawa huwa katika hatari zaidi ya kupoteza maisha kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo kushindwa kupumua kutokana na kutokomaa kwa mapafu, kupoteza joto la mwili kwa haraka, kupata uambukizo wa bakteria, kushindwa kunyonya na kupata manjano, hivyo huhitaji huduma maalum.
(a) Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na changamoto hiyo, Wizara imefanya na inaendelea kufanya jitihada mbalimbali katika kuboresha huduma kwa watoto hawa na ili kuepusha vifo hivyo kwa kutekeleza afua mbalimbali ikiwemo:-
(a) Kuwapatia wajawazito dawa ya kusaidia mapafu ya mtoto kukomaa haraka iwapo mama anatarajiwa kujifungua kabla ya wakati.
(b) Kuanzisha huduma ya Mama Kangaroo katika ngazi ya hospitali ili watoto njiti ambao hawana changamoto nyingine za kiafya watunzwe kwa utaratibu wa ngozi kwa ngozi na wazazi wao ili watunze joto mwilini. Kuanzia mwaka 2009 mpaka sasa jumla ya hospitali 63 zinatoa huduma ya Mama Kangaroo nchini.
(c) Kununua na kusambaza vifaa vya kuwahudumia watoto njiti ambao wana matatizo ya kiafya. Vifaa hivyo ni pamoja na mashine za Oksijeni, mashine za kutibu manjano yaani phototherapy machines, mashine za kufuatilia hali ya mtoto akiwa kwenye matibabu, mashine za kuongeza joto na vipima joto vya chumba cha kutibia watoto hawa.
(d) Kuendelea na mafunzo ili kuwajengea uwezo watoa huduma za afya juu ya namna ya kumhudumia mama anayetarajia kujifungua mtoto njiti kama vile mama mwenye ujauzito wa watoto pacha, mama mwenye shinikizo la damu wakati wa mimba na wenye upungufu wa damu.
(b) Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea kutoa mafunzo kwa wahudumu wa afya ngazi ya jamii, ili waweze kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masuala mbalimbali ya afya ya uzazi na mtoto, ikiwemo dalili za hatari wakati wa ujauzito, sababu zinazopelekea kuzaliwa kwa watoto njiti na umuhimu wa kuhudhuria kliniki mapema ili jamii iweze kuhamasika na kuchukua hatua stahiki na kwa wakati.
Mheshimiwa Spika, vilevile Wizara inaendelea kuwahamasisha wajawazito kumeza vidonge vya kuongeza damu, kumeza dawa za kuzuia malaria pamoja na kuwasisitiza wajawazito kupata muda wa kutosha wa kupumzika na kulala kwenye vyandarua vyenye dawa.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI aliuliza:-
Mahitaji halisi ya fedha kwa ajili ya uzazi wa mpango kwa mwaka kwa sasa ni zaidi ya shilingi bilioni 36 katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imetenga shilingi bilioni 14.
Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha zaidi ili kufikia kiasi kinachohitajika pia kuongeza kasi ya kuokoa maisha ya akina mama na watoto chini ya umri wa miaka mitano?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuwa makisio halisi ya bajeti kwa ajili ya uzazi wa mpango nchini ni shilingi bilioni 36 na kwa mwaka wa fedha 2017/2018 imetengwa shilingi bilioni 14. Hata hivyo napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kuwa shilingi bilioni 14 zilizotengwa ni sawa na ongezeko la asilimia 50 zaidi ya fedha zilizotengwa kwa mwaka 2016/2017 ambazo zilikuwa shilingi bilioni saba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sanjari na hilo, Wizara yangu inaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuhakikisha upatikanaji wa dawa za uzazi wa mpango pamoja na dawa zingine muhimu kwa kufuata taratibu maalum za mpango wa manunuzi. Kwa sasa dawa za uzazi wa mpango zinapatikana katika ngazi zote kuanzia Bohari Kuu ya Dawa hadi kwenye vituo vyote vya kutolea za afya vilivyopo Mijini na Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara imeweka mkakati maalum kwenye Mikoa na ya Simiyu, Geita, Mwanza, Shinyanga, Tabora, Kigoma na Katavi ambako matumizi ya uzazi wa mpango yako chini ya wastani wa kitaifa wa asilimia 32 kwa wanawake walio kwen ye ndoa. Kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imepanga kutumia jumla ya shilingi bilioni 22.5 kwa ajili ya uzazi wa mpango kutoka katika vyanzo vya ndani. Kiwango hiki cha fedha ni sawa na ongezeko la asilimia 60 kutoka mwaka 2017/2018.
MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza:-
Kutokana na ugumu wa maisha na mabadiliko ya mtindo wa kuishi, baadhi ya wananchi wamekata tamaa ya kuishi.
(a) Je, Serikali ina utaratibu gani wa kutoa elimu ya unasihi kwa wale wanaohitaji?
(b) Je, ni vyuo vingapi hapa nchini vinatoa wataalam wa elimu ya unasihi?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto mbalimbali za maisha zinazowakabili watu na kuwasababishia msongo wa mawazo. Changamoto hizo ni pamoja na hali ya umasikini, magonjwa, migogoro ya kifamilia, kujihusisha na matumizi mabaya ya dawa za kulevya na ulevi, ukatili na unyanyasaji wa kimwili, kijinsia na kisaikolojia. Aidha, Wizara inatambua umuhimu wa huduma za unasihi na msaada wa kisaikolojia na jamii katika kusaidia kuondokana na msongo wa mawazo. Kwa kuzingatia umuhimu wa huu wa huduma hiyo, Serikali huwatumia Maafisa Ustawi wa Jamii waliopo ili kutoa huduma hii.
Aidha, Wizara yangu kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI imefanya ugatuaji wa huduma za ustawi wa jamii kwenda katika Halmashauri ili kufikisha huduma za ustawi wa jamii ikiwemo unasihi karibu zaidi na wahitaji walio wengi. Katika ugatuaji huo jumla ya Maafisa Ustawi wa Jamii 731 tayari wameajiriwa katika halmashauri 185. Wizara itaendelea kuajiri Maafisa Ustawi wa Jamii kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kadri bajeti itakavyoruhusu ili kuwa na wataalam wa kutosha katika eneo la huduma za unasihi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vyuo 18 vinavyotoa elimu ya unasihi kati ya hivyo viwili ni vya umma na 16 ni vya binafsi. Taasisi ya Ustawi wa Jamii inatoa mafunzo ya fani ya ustawi wa jamii katika ngazi ya cheti, stashahada, shahada na shahada ya uzamili kwa lengo la kupata Maafisa Ustawi wa Jamii wenye utaalam wa kutoa huduma za unasihi. Katika mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya wanafunzi 265 walidahiliwa katika ngazi zifuatazo; cheti 192, stashahada 216, shahada 189 na shahada ya uzamili 28. Katika mwaka wa masomo 2017/2018 jumla ya wanafunzi 607 walidahiliwa katika ngazi zifuatazo; cheti 186, stashahada 210, shahada 190 na shahada ya uzamili 21. Aidha, Chuo cha Ustawi wa Jamii Kisangara kimeanza kutoa mafunzo ya wasaidizi wa ustawi wa jamii katika mwaka 2017/2018 ambapo jumla ya wanafunzi 225 wamedahiliwa katika ngazi za cheti 192, stashahada 216, shahada 189 na stashahada ya uzamili 28. Wanafunzi hawa baada ya kuhitimu watakuwa na jukumu la kutoa huduma za unasihi katika ngazi ya kata, vijiji na mitaa na katika vituo vya afya na zahanati.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA (K.n.y. MHE. RUKIA AHMED KASSIM) aliuliza:-

Kuna baadhi ya wanawake wameathirika sana na matumizi ya dawa za kuongeza makalio pamoja na matumizi ya kope na kucha bandia:-

Je, Serikali ipo tayari kufungia saloon zote pamoja na kuwachukulia hatua kali wale wote wanaotoa huduma hii?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rukia Kassim Ahmed, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kupitia Mamlaka ya Chakula na Dawa imekuwa ikidhibiti ubora, usalama na ufanisi wa bidhaa za chakula, dawa, vipodozi, vifaa na vitendanishi kupitia mifumo yake ya usajili, ukaguzi na ufuatiliaji wa ubora na usalama wa bidhaa husika zinapokuwa kwenye soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufuatilia ubora na usalama, TFDA imeweka mfumo wa kupokea taarifa kutoka kwa watumiaji na watendaji wa afya juu ya ubora na madhara yatokanayo na matumizi ya bidhaa za chakula, dawa, vipodozi, vifaa na vitendanishi. Taarifa hizo hupokelewa kupitia fomu maalum pamoja na mfumo wa kielektroniki wa upokeaji wa taarifa za madhara ya bidhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa za ubora na madhara ya chakula, dawa, vipodozi, vifaa na vitendanishi ni muhimu kwani huzisaidia Mamlaka za Udhibiti Duniani ikiwemo TFDA katika kuchukua hatua mbalimbali kuhusiana na bidhaa inapokuwa kwenye soko mfano kuiondoa kwenye soko, kuifutia usajili au kubadili matumizi ya bidhaa husika. Katika mwaka wa fedha wa 2017/2018, TFDA ilipokea kutoka kwa watumiaji na watendaji wa afya taarifa 238 za madhara yaliyohisiwa kusababishwa na matumizi ya dawa ambapo tathmini zilionesha kuwa ni salama na zinafaa kuendelea kutumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, TFDA haijawahi kupokea taarifa za madhara kuhusiana na kucha za kubandika. Kutokana na kukosekana kwa takwimu hizo, Serikali haioni sababu ya kufunga saloon zote wala kuwachukulia hatua wanaotoa huduma hii bali Wizara kupitia TFDA itaendelea kutoa elimu kwa watumiaji pamoja na kuwahamasisha watendaji wa afya umuhimu wa kutoa taarifa za ubora na madhara yatokanayo na matumizi ya bidhaa za chakula, dawa, vipodozi, vifaa, vitendanishi na vipodozi zikiwemo kucha za kubandika ili kuiepusha jamii kutokana na athari za kiafya zinazoweza kujitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara pia inatoa wito kwa watumiaji wa vipodozi kuzingatia masharti na maelekezo ya utumiaji sahihi wa vipodozi hivyo na kutoa taarifa pindi athari za matumizi ya vipodozi na vifaa vya urembo zinapojitokeza.
MHE. MAULID S. MTULIA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itanunua CT-SCAN Mashine na MRI mashine kwa ajili ya Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala ili kupunguza msongamono katika Hospatali ya Muhimbili na kuongeza ufanisi katika hospitali hii?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA NA WATOTO, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maulid Said Mtulia Mbunge wa Kinondoni kama ifuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na mwongozo ulikuwepo huduma za CT- Scan na MRI hazikuwepo kwenye hospitali za Rufaa za Mikoa. Hata hivyo, kufuatia mabadiliko ya kiuchumi na uhitaji wa huduma hizi kwa wananchi wizara yangu ilifanya mabadiliko ya mwongozo kwa kutengeneza mwongozo wa vifaa vya Radiolojia nchini wa mwaka 2018 standard Medical Radiology and imaging Equipment Guidelines – SMRIEG ambapo pamoja na mangineyo huduma za CT-SCAN sasa zinapatikana katika ngazi ya hospitali za rufaa za mikoa na huduma za MRI zitapatikana katika ngazi ya hospitali za rufaa za kanda na Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kutokana na mabadiliko hayo Serikali inakusudia kufunga CT-SCAN katika Hospitali ya rufaa ya mikoa ya Mwananyamala ambapo utelekezaji wake umeshaanza.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza:-

Je, ni lini Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Rukwa itaanza kujengwa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Rukwa unao Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Sumbawanga inayotoa huduma za rufaa kwa halmashauri nne za mkoa huo hadi sasa. Hata hivyo hospitali hiyo inayo changamoto ya ufinyu wa nafasi kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mipya ya kutolea huduma za afya ili kukidhi mahitaji ya wananchi. Kutokana na changamoto hiyo Ofisi ya Mkoa wa Rukwa imeshapata eneo jipya la ukubwa wa hekari 100 lililopo Milanzi ndani ya Manispaa ya Sumbawanga litakalotumika kwa ajili ya ujenzi wa hospitali mpya ya rufaa ya mkoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi huu utaanza baada ya kumalizika ujenzi wa hospitali za rufaa katika mikoa mipya ya Katavi, Songwe, Njombe, Simiyu na Geita.
MHE. SONIA J. MAGOGO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha au kurekebisha sheria ambazo zinaonekana kupitwa na wakati au kuchochea ukandamizaji kwa mama na mtoto?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sonia Jumaa Magogo Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikifanya tathmini na kuwasilisha baadhi ya sheria zenye upungufu ili Bunge lako tukufu likiona inafaa kuzibadili au kufanya marekebisho ya sheria hizo. Serikali imefanya marekebisho ya baadhi ya sheria na kupitia Bunge hili marekebisho mbalimbali yamefanyika naomba kutoa mifano michache. Sheria ya makosa ya Jinai Sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 kifungu cha 130(1)(2)(e) kinatoa adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela au kifungo cha maisha kwa kosa la kujiamiana na mtoto wa chini ya umri wa miaka 18.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali imefanya marekebisho ya Sheria ya Elimu ya mwaka 1978 Sura ya 353 kifungu cha 60A(1)(2) na (3), inayotoa adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela kwa mtu yeyote atakayempa mwanafunzi mimba. Marekebisho haya yanalenga kulinda haki ya mtoto wa kike kupata elimu, vilevile Serikali ilitunga Sheria ya Msaada wa Kisheria Na. 1 ya mwaka 2017 ambayo inasaidia upatikanaji wa msaada wa kisheria bure kwa wanawake na watoto wasio na uwezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na marekebisho ya sheria hizo zinazolenga kulinda haki na ustawi wa wanawake na watoto, Serikali imeandaa mpango kazi jumuishi wa Taifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto wa 2017/2018 - 2021/2022. Mpango huu wa kisekta unatekelezwa na wizara 11 chini ya uratibu ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na wadau wengine wa wanawake na watoto.

Mpango huu una eneo mahususi linaloshughulika na utekelezaji wa sheria zinazohusu wanawake na watoto.
MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. KHADIJA NASSIR ALI) aliuliza:-

Uzito mkubwa wa mwili ni dalili za mwanzo za magonjwa yasiyoambukiza:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kupambana na magonjwa haya?

(b) Je, mbali na mazoezi ni mbinu gani nyingine za kitaalamu za kupambana na vitambi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI (K.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khadija Nassir Ali, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto mnamo mwaka 2011 ilianzisha rasmi kitengo cha kupambana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa lengo maalum la kukinga na kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza. Aidha tumetengeneza mpango mkakati wa kupambana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza wa mwaka 2016-2020, ambao umewekwa malengo bayana, mikakati na utekelezaji wake ili kupambana na ongezeko la magonjwa haya. Mikakati inayotekelezwa katika mkakati huu ni pamoja na utoaji wa elimu kwa jamii kuhusu magonjwa haya na kwa kutumia njia mbalimbali ikiwemo vipeperushi, redio, runinga, mitandao ya kijamii, na nyinginezo ili kuongeza uelewa kwa jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupunguza viashiria vya hatari ambavyo vinaweza kurekebishika kwa kuhamasisha juu ya ufanyaji wa mazoezi, ulaji unaofaa, kuhamasisha kuacha matumizi ya tumbaku na pia kupunguza unywaji wa pombe kupita kiasi. Kuhakikisha huduma za uchunguzi wa awali, yaani screening for early detection, kwa magonjwa haya zinapatikana katika vituo vya afya pamoja na fanya kambi za wazi za kupima na kutibu magonjwa haya. Kutoa chanjo kwa magonjwa yanayoweza kukingwa kwa njia hii mfano, chanjo ya HPV kwa ajili ya kujikinga na saratani ya shingo ya uzazi.

Mheshimiwa Spika, ikitokea kwa bahati mbaya, ugonjwa umegundulika katika hatua za mwisho, pia eneo hili halijasahaulika. Wizara ina mkakati ambao unashughulikia uimarishaji wa huduma za tiba shufaa yaani palliative care na pia huduma ya tiba ya utengamao yaani rehabilitation services. Upo pia mkakati unaoangalia maeneo ya tafiti ili kuimarisha suala zima la upatikanaji wa takwimu sahihi za magonjwa haya.

Mheshimiwa Spika, kitambi ni dalili mojawapo ya uzito uliopita kiasi, hii si dalili njema na hupelekea magonjwa yasiyo ya kuambukiza. Njia bora ya kupambana na kitambi ni kujikinga kwa kutokukipata kwa kuhakikisha unazingatia ulaji wa vyakula unaofaa na kufanya mazoezi. Iwapo mtu akiwa ameshakipata kitambi, basi njia mojawapo ya kuondokana nacho ni kuzingatia ulaji unaofaa kwa kupunguza kiwango cha vyakula vya wanga, kupunguza kiwango cha sukari, chumvi na mafuta kwenye chakula. Kunywa maji yasiyopungua lita moja na nusu kwa siku kwa mtu mzima na kupunguza unjwaji wa pombe uliopitiliza. (Makofi)
MHE. AMINA N. MAKILAGI aliuliza:-

Wanawake 24 hufariki kila siku wakati wa kujifungua nchini:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kunusuru vifo vya Wanawake wakati wa kujifungua?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA (k.n.y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Nassor Makilagi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tafiti zilizofanywa na Taasisi ya Takwimu ya Taifa ya Mwaka 2015 zinaonyesha vifo vitokanavyo na uzazi ni 556 kwa kila vizazi hai 100,000. Hii ni sawa na vifo 32 kwa mwezi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mikakati mbalimbali ya kupunguza vifo hivi ikiwa ni pamoja na:-

(i) Kuboresha Vituo vya Afya kwa ajili ya kutoa huduma muhimu sa dharura kwa matatizo yatokanayo na uzazi na watoto wachanga. Pia kuendelea kuvipatia vituo vya kutolea huduma za afya vifaa tiba na vitendeakazi kwa ajili ya kuimarisha utoaji wa huduma za afya ya uzazi.

(ii) Kutoa mafunzo mbalimbali ya huduma muhimu za dhahrura kwa matatizo yatokanayo na uzazi na watoto wachanga kwa watoa huduma za afya ili waweze kutoa huduma zenye viwango kwa jamii. Aidha, mafunzo haya pia hutolewa kwa wahudumu wa afya ngazi ya jamii kama njia ya kushirikisha jamii ili waweze kusaidia katika kupunguza vifo hivyo.

(iii) Kuhakikisha upatikanaji wa dawa muhimu kwa ajili ya uzazi salama ikiwemo dawa ya oxytocin kwa ajili ya kuzuia mama mjamzito kutokwa na damu nyingi wakati na baada ya kujifungua na dawa ya magnesium sulphate kwa ajili ya kuzuia kifafa cha mimba.

(iv) Kuimarisha huduma za rufaa kwa kuzambaza magari ya kubebea wagonjwa. Aidha, mwishoni mwa mwaka 2016 magari 67 yalitolewa kwa Halmashauri mbalimbali ili kusaidia kuimarisha huduma hizi.

(v) Wizara ilitoa mafunzo elekezi nchi nzima kwa watoa huduma wa afya ngazi za Mkoa na Halmashauri kuhusu upitiaji na utoaji wa taarifa za vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga ili kutambua tatizo lililotokea na kuweka mikakati ya kuzuia vifo hivyo visitokee tena.

(vi) Kushirikisha jamii kutambua kuwa inayo wajibu wa kutengeneza mikakati na Kanuni zitakazowawezesha kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na vifo vya watoto wachanga katika jamii husika.
MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:-

Serikali imekuwa ikihimiza wananchi kuchangia damu na kuihifadhi katika benki za damu kwa ajili ya watu wenye uhitaji.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuanzisha utaratibu maalum wa kuvuna viungo kama vile figo na moyo kutoka kwa watu waliopata ajali na wapo kwenye hali ya kupoteza maisha au kutoka kwa watu walioridhia kutolewa viungo hivyo na kuvihifadhi kwa ajili ya Watanzania wenye uhitaji wa viungo hivyo?.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rose Cyprian Tweve Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ipo katika hatua za mwisho za kuandaa Muswada wa Sheria ya Uvunaji, Utunzaji, Usafirishaji na Upandikizaji wa viungo vya binadamu ikiwemo, Figo, Moyo, Maini, Mapafu, sclera ya macho, Uroto, IVF, pamoja na Stem cells itakayoweka utaratibu mzuri wa namna ya kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria itaelekeza vitu vya kuzingatia kwa mpokeaji na mtoaji wa viungo. Sheria hii itaweka utaratibu kwa watu wanaoridhia kutolewa viungo vyao pindi wanapokaribia kupoteza maisha ikiwa mchangiaji (donor) huyo atakuwa ameridhia viungo vyake vitumike kwa ajili ya jamii inayohitaji viungo hivyo pindi akipoteza maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu inaheshimu haki za binadamu ikiwemo haki ya kuishi, mtu kupata ajali na kutolewa viungo vyake litafanywa pale ambapo mhusika atakuwa ameridhia akipata ajali na akawa hana uwezo wa kupona atolewe viungo, basi hatua za kisheria na kitabibu zitatumika ili kutoa viungo hivyo na kuvihifadhi kwa ajili ya matumizi ya mtu atakayehitaji.
MHE. JOYCE B. SIKOMBI aliuliza:-

Kumekuwa na wimbi kubwa la wazee ambao wanaoishi mtaani katika mazingira magumu.

Je, Serikali imejipanga vipi kuweza kusaidia wasiendelee kuteseka?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu Swali la Mheshimiwa Joyce Bita Sokombi (Viti Maalum) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuweka mikakati madhubuti kuhakikisha kuwa wazee wote nchini wanafurahia maisha ya uzee hasa tukizingatia kuwa wazee ni hazina ya Taifa. Katika kuhakikisha kuwa haki, ustawi, ulinzi na usalama wa wazee unaimarishwa, Serikali kupitia mamlaka za Serikali za Mitaa imekuwa ikifanya utambuzi na uandikishaji endelevu wa wazee wasiokuwa na uwezo wa kujimudu kimaisha katika jamii na kuwapatia huduma za msingi za ustawi ikiwemo vitambulisho vya matibabu bila malipo, malazi katika makazi ya wazee wasiojiweza, pamoja na msaada wa kisaikolojia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia Machi, 2020 kuna wazee wasiojiweza 349 (wanawake 149 na wanaume 200) wanahudumiwa na Serikali kwenye Makazi 13 ya wazee nchini. Wazee wale ambao hawana watoto, ndugu wala jamii wa karibu wa kuwahudumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hakuna tathmini rasmi kitaifa iliofanyika kuwatambua wazee wanaoishi mitaani kwani miongoni mwao hutokea katika familia na jamii zao kuja mitaani kuomba mchana na kurudi makwao jioni au kulala pembezoni mwa maduka na katika masoko. Aidha, nitumie fursa hii kutoa wito kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuendelea kuwatambua wazee na kuwaunganisha na huduma za msingi, pia familia na jamii kutekeleza wajibu wao wa kutoa matunzo kwa wazee hususan wale wasiojiweza.
MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza:-

Elimu ya Afya ya Uzazi ni muhimu sana kwa vijana wa kike na kiume katika kuepuka mimba zisizo za lazima.

Je, Serikali imejipangaje kuwahabarisha vijana ili kupunguza mimba zinazozuilika?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau imeaandaa mitaala ya kuwafundishia watumishi wa afya pamoja na vijana kuhusu afya ya uzazi kwa vijana ili kuwajengea uwezo wa kujitambua hasa kuhusu hatua za makuzi wakati wa kubalehe na namna ya kuhimili mihemko ili wasijihusishe na masuala ya ngono katika umri mdogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mafunzo haya huwajengea weledi na stadi za maisha vijana wetu hivyo kuwasaidia kuzingatia masomo zaidi na kujipanga vizuri ili kufikia ndoto zao za maisha. Aidha, Wizara kwa kushirikiana na wadau, mwaka 2018 ilizindua Jukwaa la Vijana la SITETEREKI lenye maudhui mahususi ya kumuelimisha kijana awe na mtazamo chanya wenye kumuwezesha kupata taarifa na huduma muhimu za uhakika kuhusu afya ya Uzazi kwa Vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kwa kushirikiana na Wizara nyingine ikiwemo Wizara ya Elimu pamoja na Wadau wa maendeleo imeandaa Agenda ya Kitaifa ya Afya kwa Vijana na Uwekezaji (NAIA) yenye afua mtambuka zinazowahusu vijana hasa wenye umri wa miaka 10 hadi 19. Ajenda hiyo ilikuwa izinduliwe mwezi Machi mwaka huu, lakini kutokana na tishio la ugonjwa unaotokana na virusi vya Corona zoezi hilo limeahirisha kwa muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeona ni vema kuileta mikakati yote inalenga vijana pamoja na kuitengenezea ajenda moja. Ajenda hii imejikita katika maeneo sita ambayo ni eneo la kwanza ni Kuzuia maambukizi ya VVU, eneo la pili ni kuzuia mimba za utotoni na utoro wa shule, eneo la tatu ni Kuzuia unyanyasaji wa jinsia, kimwili na kisaikolojia, eneo la nne ni kuboresha lishe ya vijana; eneo la tano ni kuhakikisha wavulana na wasichana wanabaki shuleni na eneo la sita ni kuwajengea stadi za maisha kupambana na mazingira yanayowazunguka, ni Imani yangu kuwa, tukitekeleza kwa ufanisi afua zilizomo kwenye nguzo hizi tutakuwa tumemwezesha kijana wa Kitanzania kupata elimu ya afya ya uzazi kwa kiasi kikubwa hivyo kuwafanya kuwa rasilimali muhimu katika kuujenga uchumi wa nchi na kuweza kufikia lengo letu la kuwa nchi yenye uchumi wa kati.
MHE. MARIAM M. NYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha jengo la hosteli ya madaktari watarajali katika Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma lililoanza kujengwa mwaka 2014/2015?
WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Madalu Nyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni moja katika mwaka wa fedha 2022/2023 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa jengo la hosteli ya madaktari watarajali (interns) katika Hospitali ya Mkoa Ruvuma.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa hosteli hii utaendelea mara tu fedha hizi zitakapokuwa zimetolewa na tunatarajia ujenzi huu utakamilika ifikapo Juni, 2023.
MHE. SUBIRA K. MGALU aliuliza: -

Je, ni lini Hospitali ya Rufaa Tumbi na Hospitali za Wilaya za Mkoa wa Pwani zitapokea vifaa tiba ikiwa ni sehemu ya fedha za kupambana na UVIKO-19?
WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Subira Khamis Mgalu, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani - Tumbi imeshapokea vifaa tiba 74 kati ya 77 vilivyoagizwa kwa fedha za kupambana na UVIKO-19, hii ni sawa na asilimia 94 ya vifaa vyote vilivyoagizwa ikiwemo mashine ya CT Scan. Kazi ya kusimika vifaa hivi inaendelea na inatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, 2022.

Mheshimiwa Spika, aidha, kwa upande wa Hospitali za Wilaya, ujenzi wa majengo ya huduma za dharura yaani EMD na majengo ya huduma za wagonjwa waliopo kwenye uangalizi maalum yaani ICU unaendelea. Hivyo vifaa tiba kwa ajili ya hospitali hizi vitafikishwa mara baada ya ujenzi kukamilika.
MHE. HASSAN Z. KUNGU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalinda watumiaji wa cyanide kama mbadala wa zebaki?
WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Zidadu Kungu, Mbunge wa Tunduru Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatumia njia mbalimbali kuwalinda watumiaji wa cyanide kuzuia athari za kiafya zisitokee wakati wa kutumia kemikali hizi ikiwa ni pamoja na: -

(a) Kuelimisha wachimbaji juu ya madhara yanayotokana na matumizi ya cyanide na namna ya kujikinga na madhara yake. Pia kuwaelimisha kufika vituo vya kutolea huduma za afya mapema kupata matibabu wanapopata madhara.

(b) Kufanya upimaji wa afya za wafanyakazi maeneo ya migodini.

(c) Kutumia njia nyingine katika uzalishaji wa dhahabu katika migodi iliyopo hapa nchini kama direct smelting na njia nyingine mbadala.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha huduma za afya kwa Wazee badala ya kutumia Dirisha la Wazee ambalo linawatesa?
WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimuwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuimarisha huduma za afya kwaa wazee. Kwa miaka mingi wazee wamekuwa wakipatiwa huduma mahsusi kwa kupitia madirisha maalum ya huduma za afya kwa wazee yaliyotengwa katika vituo vya kutolea huduma za afya. Katika kuimarisha huduma za afya kwa wazee, Wizara katika Mwaka huu wa fedha 2022/2023 imepitishiwa muundo mpya ambao umewezesha Wizara kuanzisha seksheni ndani ya Kurugenzi ya Tiba inayoshughulika na Huduma za Afya ya Wazee, Huduma za Utengamao na Huduma za Tiba Shufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, chini ya Seksheni hii mpya, Utaratibu wa huduma mbalimbali za afya ya wazee utafanyika na maboresho ya huduma za afya kwa wazee yatapokelewa na kuchakatwa na kupatiwa majawabu kwa wakati. Rasimu ya mwongozo wa utekelezaji wa mkakati wa huduma za afya kwa wazee ipo katika ngazi ya maboresho hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uzee na kuzeeka havikwepeki, Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kuwaenzi wazee wetu.
MHE. LUCY J. SABU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupunguza vifo vya akina mama wajawazito?
WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, niruhusu kwa kuwa leo ni siku ya Wauguzi Duniani, nitumie Bunge lako Tukufu kuwashukuru wauguzi wote nchini Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya katika kuwahudumia wagonjwa. Tunafahamu kwamba asilimia 80 ya huduma katika hospitali zinafanywa na wauguzi, na tunatambua kwamba wana mzigo mkubwa. Tutaendelea kuajiri watumishi wauguzi wengi tutaendelea kuboresha mazingira ya kufanya kazi kwa wauguzi wote Tanzania. Tunawaomba watimize wajibu wao kwa kuzingatia viapo vyao ambao ni kuokoa maisha.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy John Sabu, Mbunge wa Viti Maalum, Vijana, Mkoa wa Simiyu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatoa elimu kwa Umma hususan kwa akina mama wajawazito kuhusu viashiria vya hatari kupitia njia mbalimbali ikiwemo vyombo vya habari na wakati wa mahudhurio ya kliniki. Aidha, Serikali inasomesha wataalam mbalimbali wa afya ya uzazi katika ngazi ya ubingwa na inaendelea kuimarisha miundombinu katika vituo vya kutolea huduma za afya na kuhakikisha upatikanaji wa dawa na vifaatiba pamoja na kuhakikisha huduma za mama wajawazito zinatolewa bure.
MHE. FLORENT L. KYOMBO aliuliza: -

Je, Serikali haioni kuwa kufutwa kwa Form 2c katika huduma ya Bima ya Afya inakosesha mgonjwa kupata dawa iliyokosekana hospitali aliyotibiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT FESTO J. DUGANGE) K.n.y. WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Florent Laurent Kyombo, Mbunge wa Nkenge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, maamuzi ya Serikali ya kusitisha matumizi ya fomu za dawa (Form 2C) katika vituo vya kutolea huduma za afya yalifanyika kwa kuzingatia manufaa yake, ikiwemo utekelezaji wa maelekezo ya watoa huduma wote wa Serikali. Kwamba kuwe na utaratibu wa kuanzisha maduka ya dawa yanayomilikiwa na hospitali na hivyo kuongeza mapato ya ndani ya hospitali. Pia kuepusha usumbufu kwa wananchi wa kutafuta dawa nje ya hospitali na hivyo kusabisha lawama zisizo za lazima kwa Serikali. Vilevile na kuepusha vitendo vya udanganyifu vinavyofanywa katika eneo la dawa dhidi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Wizara imevielekeza vituo vya kutolea huduma kuweka utaratibu wa Mgonjwa kupata dawa iliyokosekana hospitali aliyotibiwa ili kuepusha usumbufu kwa wananchi. Ahsante.