Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Ummy Ally Mwalimu (73 total)

MHE. KEMIREMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Nashukuru kwa maelezo mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini nasikitika kusema hajajibu swali langu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mkoa wa Mwanza wanapata taabu kwa vipimo vya x-ray na CT-Scan na inawabidi waende kwenye Hospitali za Private ambazo ni gharama kubwa sana kufanya vipimo hivi. Swali langu: Je, ni lini Serikali itanunua machine ya CT-Scan na x-ray kwa hospitali yetu ya Mwanza ya Sekou Toure?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kemirembe, Mbunge wa Viti Maalum, Mwanza kama fuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, alichojibu Mheshimiwa Naibu Waziri kinabaki kuwa ni sahihi. Tuna mradi wa Orion kwa ajili ya kununua vifaa tiba na kuvisimika katika hospitali zote za Rufaa nchini ikiwemo Hospitali ya Rufaa ya Sekou Toure, Mwanza. Tumepata fedha, juzi Mheshimiwa Rais katika ile fedha ya kufanya Semina Elekezi kwa Mawaziri shilingi bilioni 2.8 itatumika kwa ajili ya kununua vifaa hivi. Tulikwama muda mrefu kwa sababu hiyo fedha haijapatikana. Fedha imeshatolewa. Kwa hiyo, lini? Tayari, anytime, soon, tutaweza kusimika hivi vifaa katika Hospitali za Rufaa zote za Mikoa Tanzania.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Kemirembe tunakuomba sana, tunajua wananchi wanatumia gharama kubwa kufanya hivi vipimo katika hospitali binafsi na lengo letu ni kuwapunguzia mzigo Watanzania. Hili tunalifanya kabla ya mwaka huu wa fedha wa 2015/2016 haujaisha.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Kwa kuwa wanawake wengi sana wanaoishi vijijini hasa katika Mkoa wetu wa Iringa, wamekuwa wakipata shida sana wanapotafuta msaada wa kisheria; na kwa kuwa mashirika haya mengi yako mijini.
Je, Serikali inawasaidiaje wananchi ambao wanakaa mbali na miji ili angalau hata kupeleka mobile elimu ili waweze kufikiwa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wanawake wengi walioko vijijini wanakabiliwa na changamoto ya kupata msaada wa Sheria, lakini nataka nimthibitishie kwamba kwa sasa hivi Waziri wa Katiba na Sheria tayari ameshaleta mapendekezo ya Kutunga Sheria ya Msaada wa Kisheria ambapo itahakikisha msaada wa kisheria unapatikana kwa wananchi wote wenye mkahitaji, wakiwemo wanawake walio vijijini. Kwa hiyo, ni suala ambalo tayari Serikali ya Awamu ya Tano inalifanyia kazi na tunataka kumuahidi kwamba ndani ya siku chache tutakuwa na sheria, hivyo wanawake wataweza kupata.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili; tayari tunazo NGOs mbalimbali ambazo zinafanya kazi ya kutoa Msaada wa Sheria kwa wanawake, ikiwemo Chama cha Wanasheria Wanawake na Chama cha Wanawake Wanahabari. Kwa hiyo, tunazo taasisi mbalimbali ambazo zinatoa msaada wa sheria kwa wanawake.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huu umegharimu shilingi bilioni tano kwa hospitali ya Bombo, Tanga, Mwananyamala na kitengo cha MOI. Je, Serikali ilifanya utafiti wa gharama halisi za mifumo hii kutoka kwenye taasisi zingine ambazo zimefunga mfumo huu kwa gharama nafuu sana mfano hospitali ya Haydom imefunga kwa gharama ya shilingi milioni 150, Hospitali ya Seliani imefunga kwa gharama ya shilingi milioni 120. Je, mlifanya utafiti?
Swali la pili; kuna tafiti zimefanyika katika kufunga mfumo huu kwenye hospitali za Wilaya inagharimu kati ya shilingi milioni 28 mpaka 35 na hospitali za Rufaa inagharimu kati ya shilingi milioni 75 mpaka milioni 200. Nataka kupata taarifa ya Serikali, hapa hakuna harufu ya ufisadi kwa Hospitali 5 kufunga mfumo kwa shilingi bilioni 5 na hapo hapo, Hopsitali ya Bombo ya Tanga ilishakuwa funded na Wajerumani kufunga mfumo huu lakini kupitia NHIF tena wamepewa fedha katika hii bilioni 5.
Je, mko tayari kufanya utafiti? Kufanya Special audit? Kuleta taarifa hapa na wahusika wawajibishwe?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze kwa maswali yake ya nyongeza. Pili nimpe taarifa tu kwamba kuna tofauti ya mifumo inayofungwa kwenye hospitali za Wilaya na mfumo huu ambao umefungwa kwa ufadhili wa mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.
Katika hospitali za Wilaya, tunafunga Electronic Payment Systems tu! Hatufungi Comprehensive, Health Management Information System, ambayo yenyewe inaunganisha hadi na taarifa za Bima ya Afya na taarifa za Vizazi na Vifo lakini pia taarifa za claims – Online Claims System ambayo inawafanya hospitali husika waweze ku-submit maombi ya madai yao ya Bima ya Afya kwa Bima ya Afya kwa njia ya mtandao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo mifumo tunayofunga ni tofauti sana kati ya hii inayofungwa kwenye Hospitali za Wilaya, Hospitali za Mikoa na huu mfumo mahsusi ambao umefungwa katika hizi hospitali 5 kwa majaribio na taasisi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), labda nimwambie tu kwamba kwa kufanya huu utaratibu wa kufunga mifumo ya kielektroniki, Serikali imeweza kufanya mapinduzi makubwa katika makusanyo ya fedha zinazopatikana kwa kutoa huduma za afya kwa wananchi nchini. Mimi hapa ninayezungumza nimekuwa pioneer wa wazo hili ndani ya Serikali, hivyo ninafahamu mifumo hii na ninaelewa tunachokifanya ndani ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie kwamba mfumo uliofungwa kwa ufadhili huu wa NHIF umekuja pamoja na source codes, kitaalam ndiyo mfumo halisi, ndiyo ile Architecture halisi ya mfumo huo. Kwa hiyo, kazi iliyobaki sasa ni kwa taasisi ya NHIF kuchukua hizi source codes na kuwekeza kwenye switch zile za mtandao kuwekeza kwenye computer, kwa ajili ya kutanua mfumo huu kwenye hospitali nyingine mbalimbali. Kwa hivyo, kwa kuwa, tuna source codes zetu wenyewe sasa tuna uwezo wa kufunga mfumo huo kwa gharama ya chini zaidi kwenye hospitali nyingine zote nchini na huko ndiko tunakoelekea.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyozungumza hapa, mwezi wa sita taasisi ya Bill & Melinda Gates imeamua kumtuma mke wa Bill Gates, Melinda Gate, kwa ajili ya kuja kuzungumza na Naibu Waziri wa Wizara hii, tayari kuwekeza kwa kiasi kikubwa kwenye mifumo ya taarifa za afya nchini. Haya ni mafanikio ambayo yanakuja kutokana na initiative tuliyoifanya ndani ya Serikali ya kuwekeza kwenye mifumo ya ki-electronic.
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza. Tatizo la Benki ya Wanawake limekuwa ni kubwa katika mikoa yote, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, ni kwanini Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto isikae na kukubaliana na benki ambazo zinapatikana kwa kila mkoa kama NMB, CRDB na NBC ili waweze kuweka angalau dirisha moja kwa kila mkoa kuweza kutoa huduma hizi?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kweli kwa sababu msema kweli ni mpenzi wa Mungu. Lengo la benki lilikuwa ni kufikisha huduma za mikopo yenye riba nafuu kwa wanawake hasa walio vijijini. Katika jitihada ambazo zimefanyika hatukuweza kwa kweli kufikia lengo hilo ni lazima nikiri hilo. Nimshukuru sana Mheshimiwa Azza kwa wazo zuri tunalipokea na tayari nimeshapata baadhi ya benki ambazo ziko tayari kushirikiana na Benki ya Wanawake ili sasa tuweze kufungua dirisha la Benki ya Wanawake katika benki ambazo ziko katika mikoa na wilaya mbalimbali. Kwa hiyo, kwa kweli naamini ndani ya miezi mitatu tutaweza kuja na suluhisho maalum la kuhakikisha huduma za Benki ya Wanawake zinafika hasa kwa wanawake walio vijijini.
MHE. MARTHA J. UMBULLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwa umuhimu huohuo wa wanawake wa Mkoa wa Morogoro kupata mikopo kutoka Benki ya Wanawake, Mkoa wetu wa Manyara, wanawake wengi ni wa kutoka jamii ya wafugaji na jamii ya wafugaji hawana elimu pana ya kukopa katika vyombo vya benki hasa tutakapokuwa tumefikiwa na Benki ya Wanawake. Je, Wizara ina mkakati gani kuhakikisha kwamba inaandaa mafunzo ya ujasiriamali pamoja na elimu ya uelewa ili wanawake wa jamii ya kifugaji nao waweze kunufaika na Benki ya Wanawake?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tuna changamoto ya kuwafikia wanawake ambao wako katika jamii za wafugaji lakini pia wanawake wenye ulemavu. Kwa hiyo, ni jambo ambalo tayari nimeshatoa maelekezo kwa Benki ya Wanawake kwamba wakati tunapotoa huduma zetu pia lazima tuwe na huduma maalum kwa wanawake walio pembezoni ikiwemo walio katika jamii za wafugaji. Pia nimeshatoa maelekezo kwa Benki ya Wanawake, tuwe na huduma mahsusi kwa ajili ya wanawake wenye ulemavu na nataka kumthibitisha Mheshimiwa Umbulla na Waheshimiwa Wabunge wanawake wengine ili msiweze kusimama tena kuuliza maswali ya nyongeza kwamba kuwawezesha wanawake kiuchumi ndiyo kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Tano, tunapozungumzia masuala ya usawa wa jinsia, tutajikita tu katika kuwawezesha wanawake kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii imetokea kutokana na takwimu ambazo tunazo kwamba, kwa mfano wanawake ambao wanatumia huduma mbalimbali za benki ni asilimia 51 ukilinganisha na wanaume wanaotumia huduma za benki ni asilimia 63. Kwa hiyo, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa sababu ni Mjumbe wa High Level Panel on Women’s Economic Empowerment (Jukwa la Kimataifa la Kuwawezesha Wanawake Kiuchumi), ameanzisha jitihada mahsusi za kuhakikisha kwamba wanawake wa Tanzania hasa walio vijijini wanafungua akaunti katika benki mbalimbali nchini, ameanza na akaunti inayoitwa Malaika Account. Lengo la Mama Samia pia ni kutoa elimu kwa wanawake ili waweze kujua masuala mbalimbali ya ujasiriamali na kauli mbiu yake anasema „usinipe samaki nipe nyavu na elimu ili niweze kuvua‟. Kwa hiyo, tunampongeza sana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, tunaamini kupitia yeye tutaweza kuwafikia wanawake mbalimbali hasa walio vijijini.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini tatizo lililoko Hospitali ya Rufaa ya Mbeya ni dogo sana ukilinganisha na tatizo kubwa sana lililoko katika Hospitali ya Mkoa wangu wa Arusha, Hospitali ya Mount Meru. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Mount Meru hatuna CT-Scan, hatuna MRI Machine, hatuna X-Ray Processor na Ultrasound with Doppler. Kwa hiyo, wananchi wa Mkoa wa Arusha wamekuwa wakitaabika sana kwa sababu Hospitali ya Mount Meru ndiyo hospitali yetu tegemezi. Je, Serikali ina mpango gani wa kushughulikia tatizo hili katika Hoapitali ya Mount Meru haraka iwezekanavyo?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme, tuna mradi wa kuboresha huduma za kiuchunguzi katika Hospitali zetu zote za rufaa za kanda na hospitali za rufaa za mikoa. Kwa hiyo, katika bajeti yangu ya 2016/2017 tumetenga kiasi cha takriban shilingi bilioni 9 kwa ajili ya kununua vifaa hivyo na kati ya hospitali ambazo tutazipa kwa mfano kama CT-Scan ni pamoja na Hospitali ya Rufaa ya Mount Meru - Arusha.
Mheshimiwa Naibu Spika, niweke wazi, vifaa kama X-Rays ni kwamba hospitali zenyewe nazo zina wajibu wa kununua vifaa tiba na sasa hivi wanaweza wakatumia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kuomba mkopo na kununua vile vifaa tiba ambavyo gharama yake siyo kubwa. Vifaa kama CT-Scan na MRI tutaweza kuwapatia kwa kupitia mradi wa Orion.
MHE. AYSHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Tatizo la Hospitali ya Rufaa ya Mbeya ni sawasawa na matatizo yanayoikabili Hospitali ya Rufaa ya Singida. Je, Serikali ina mpango gani wa kuiboresha Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ikiwa ni pamoja na kuipatia watumishi wa kutosha, vifaa tiba kama X-Ray na kufanya ukarabati mkubwa wa majengo ya hospitali hiyo? Ahsante.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ili pia kutowasimamisha Waheshimiwa Wabunge wengine, kupitia Mradi wa Orion kama nilivyosema tumetenga shilingi bilioni 9 kwa ajili ya kununua vifaa tiba, hasa vifaa vya uchunguzi katika Hospitali za Rufaa ikiwemo Sekou Toure na Singida Regional Referal Hospital, Iringa Regional Referal Hospital na Musoma Regional Referal Hospital. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa hawa wanaotoka katika mikoa hii wasisimame. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili kwamba ni lini sasa tutaweza kupeleka watumishi wa kutosha, kama nilivyosema tumeomba kibali cha kuajiri watumishi 30,000 katika sekta ya afya na tumeruhusiwa kuajiri watumishi 10,000. Kwa hiyo, mara taratibu zitakapokamilika, basi tutaweza pia kupeleka Madaktari Bingwa na watumishi wengine wa sekta ya afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida.
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja dogo la nyongeza. Nikija katika swali la msingi ambalo limeulizwa na Mbunge wa Mbeya Mjini ambalo mimi nimeletewa majibu yake hapa, naomba kuuliza swali dogo moja tu la nyongeza kwa sababu sikuuliza swali la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake ya matumaini ambayo ametupatia sisi Wana-Mbeya kwamba mwakani suala hili litakuwa limekamilika katika suala la msingi la Mbunge wa Mbeya Mjini. Nilitaka kujua tu Hospitali hii ya Rufaa ya Mbeya kwa sababu ndiyo inayohudumia Ukanda mzima wa Nyanda za Juu Kusini, congestion ya wagonjwa ni kubwa sana, Serikali ina mkakati gani katika kuongeza majengo ili kupata bed capacity? Ahsante.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa kwa kupigania maendeleo ya Mkoa wa Mbeya na maendeleo ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini. Nimetembelea Mbeya na nimemwona Mheshimiwa Dkt. Mary akishiriki katika shughuli mbalimbali za kimaendeleo, za afya, elimu na za kuwawezesha wanawake kiuchumi. Nakupongeza sana kwa hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikijibu swali lake, ni kweli Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya inahudumia mikoa takriban minne; Mikoa ya Mbeya, Songwe, Njombe, Iringa, Ruvuma, Rukwa na Katavi. Kwa hiyo, kwetu sisi ni hospitali ambayo tunaipa kipaumbele cha kutosha. Katika kumthibitishia hili, tunafanya mipango ya kuongeza kujenga jengo kwa ajili ya kuhudumia wanawake wajawazito katika kile Kitengo cha Hospitali ya Wanawake cha Meta.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutaanza kwanza kuongeza jengo kwa ajili ya akina mama wajawazito halafu tutapanua miundombinu, tunataka pia Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya itoe huduma pia ya matibabu ya saratani badala ya wananchi kuhangaika kwenda Dar es Salaam. Tunataka huduma kama hizo za saratani pia ziweze kupatikana na Hospitali ya Rufaa ya Mbeya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumthibitishia Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa, kwa sababu makusanyo ya Serikali ya Awamu ya Tano ni makubwa sana, tuna matumaini kwamba tutapata hela kama tulivyoweka katika bajeti yetu ili tuweze kutekeleza mipango hiyo ya miradi ya maendeleo ambayo tumeipanga.
MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Naomba niulize maswali mawili madogo tu ya nyongeza.
Kwa kuwa ugonjwa huu wa fistula umeleta athari sana kwa wanawake wakiwemo hata wanawake wa Iringa pamoja na Njombe, kutokana hasa na ukosefu wa vifaa vya kujifungulia na miundombinu migumu sana ambayo wanawake wamekuwa hawavifikii hata vituo vya afya wala zahanati.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wanawake kwanza hawajifungulii majumbani na vifaa kuwepo katika zahanati na vituo vya afya hasa vilivyopo katika vijiji vyetu huko ndani kabisa?
Swali la pili, je, Serikali imebaini ni kwa kiasi gani wanawake wameathirika kutokana na ugonjwa huu wa fistula?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, niruhusu kwanza niseme jambo moja kwa ufupi kwamba ugonjwa wa fistula ni ugonjwa ambao unasababisha kuwepo kwa tundu lisilo la kawaida kati ya uke na kibofu cha mkojo au kati ya uke na njia ya kutolea haja kubwa.
Jambo la pili ambalo ningependa kulifafanua ni kwamba, ugonjwa huu hausababishwi na laana, kurogwa au mwanamke kutembea na wanaume wengi wakati wa ujauzito. Nimeona niliseme hili kwa sababu wanawake wengi wamekuwa ni wahanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali yake mawili ya nyongeza; kwamba tuna mikakati gani sasa ya kuhakikisha wanawake wanajifungulia katika vituo vya afya. Tulieleza wakati tunawasilisha bajeti yetu hapa, la kwanza ni kwamba tutaendelea kutoa elimu kwa wanawake wajawazito kuhakikisha wanahudhuria kliniki wakati wanapokuwa wajawazito na especially tutahamasisha wale wanawake wa kuanzia miezi miwili.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo tutalifanya ni kuhakikisha kwamba tunaweka huduma za upasuaji wa dharura katika vituo vya afya. Nimesikiliza michango ya Waheshimiwa Wabunge wakati wa mjadala huu ambao unaendelea wa bajeti ya Serikali hasa Wabunge wa chama changu, wanawake wa Chama cha Mapinduzi, wameongea kwa sauti kubwa sana kuhusu umuhimu wa kuboresha huduma za upasuaji wa dharura.
Kwa hiyo, nataka kumthibitishia Mheshimiwa Ritta Kabati kwamba bajeti ya Wizara ya Afya inayokuja itahakikisha tunaweka vichocheo vya kuwafanya wanawake wahudhurie kliniki na nilishasema, tutatoa vifaa vya kujifungulia kwa wanawake 500,000 kuanzia mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, madhara ya ugonjwa huu wa fistula. Yapo madhara ya kiafya, madhara ya kiuchumi na kijamii. Ya kiafya kama nilivyosema, mwanamke anatokwa na mkojo bila kujizuia, lakini pia haja kubwa inatoka katika njia ya uke. Kwa hiyo, hayo ni madhara ya kiafya na asilimia 85 ya wanawake ambao wanapata fistula wanapoteza watoto.
Mhehimiwa Naibu Spika, madhara makubwa ni ya kiuchumi na kijamii. Wanawake wengi wanaachwa na wanaume wao kwa sababu tu wamepata ugonjwa huo wa fistula, lakini wanawake hawa hawawezi kufanya shughuli za kujiletea maendeleo yao kwa sababu wana harufu, hawezi hata kufungua duka la maandazi au kigenge.
Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa ambalo nataka kuwathibitishia wanawake, ugonjwa wa fistula unatibika na matibabu yake yanapatikana katika hospitali zetu. Lengo la Wizara ya Afya ni kuhakikisha wanawake hawapati fistula, lakini kama wakipata basi wapate matibabu. Kwa hiyo, katika Hospitali zetu zote za Rufaa za Mikoa tutahakikisha huduma za upasuaji wa matibabu ya fistula zinapatikana. Nakushukuru.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la fistula limekuwa likiongezeka kadri miaka inavyoenda hususan maeneo ya vijijini; je, Serikali ina mpango gani wa kuelimisha wakunga wa jadi ili kupunguza tatizo la fistula na vifo vya mama na mtoto?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Maria Kangoye, Mbunge Viti Maalum (Vijana) kwa kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri sitawatendea haki Watanzania kama sitakiri kwamba fistula inawapata wanawake walio katika hali ya chini ambao wako vijijini na kwa sababu ya uhaba wa miundombinu wa vituo vya afya, uhaba wa wataalam, pia usafiri wa kutoka pale nyumbani kwenda kituo cha afya na wanawake wa mijini ambapo kunakuwa na msongamano wa watu katika upatikanaji wa huduma za afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Kangoye anataka kujua, Serikali tutawahamasisha au tutawashirikisha vipi wakunga wa jadi ili waweze kuhakikisha kwamba na wenyewe wanashiriki katika kuokoa vifo vya akina mama wajawazito?
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, asilimia 48 ya wanawake wa Tanzania bado wanajifungulia majumbani maana yake wanajifungulia kwa wakunga wa jadi. Kwa hiyo, Wizara ya Afya itaendelea kuhakikisha tunawapa elimu na kuwaelewesha kwamba wasitoe huduma za kujifungulia kwa hawa wanawake wanaowafuata; wao wawe kama ni sehemu ya rufaa. Mwanamke akienda kwa mkunga wa jadi, basi yeye ampeleke au amhamasishe kumpeleka katika kituo cha afya. Ni jambo ambalo tutalifanyia kazi, lakini pia tumekuwa tukitoa mafunzo kwa wakunga wa jadi jinsi gani ya kuwahudumia wanawake wajawazito ili tuweze kuepusha vifo vya akina mama wajawazito.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nilisema, tumeamua kuanza kutoa vifaa vya kujifungulia kwa wanawake wajawazito ili kuwa kichocheo cha wao kwenda sasa kwenye vituo vya afya vya kujifungulia badala ya kujifungulia majumbani. Ni jambo ambalo tutalipa kipaumbele. Niwathibitishie Wabunge wenzangu wanawake, mimi ni mama; nimepita labour mara mbili. Kwa hiyo, suala la uzazi salama kwa mwanamke ni suala la kipaumbele kwangu.
MHE. BAHATI ALI ABEID: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo hili la fistula wanawake wanapolipata, huwa wanatumia pesa nyingi ili kupona. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kwa wanawake wanaopata tatizo hili wakatibiwa bure?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Nimshukuru sana Mheshimiwa Bahati Abeid, Mbunge wa Jimbo la Mahonda kwa swali lake zuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, sera yetu ya afya inasema mwanamke mjamzito ndiye anatakiwa kupata matibabu bure; na huduma hizi za fistula especially suala la upasuaji zinafanyika baada ya siku 40 baada ya mwanamke kujifungua. Kwa hiyo, niseme tu tumelibeba. Naomba nilipokee, haliko kisera, lakini kwa sababu kama unavyosema ni jambo ambalo linawaathiri wanawake wengi hasa wa vijijini, nitashauriana na wenzangu tuone ni jinsi gani tutatoa matibabu bure kwa wagonjwa wa fistula. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Hospitali ya CCBRT, wao wanatoa matibabu bure kwa wagonjwa wa fistula. Kwa hiyo, ni changamoto kwetu sisi wa Serikali pia kuhakikisha kwamba na matibabu hayo bure ya fistula yanapatikana katika Hospitali za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa ni kwamba ule upasuaji unachukua saa sita na daktari anatakiwa ainame kwa saa sita.
Kwa hiyo, tutaangalia ni jinsi gani tutakuja na incentive package ya jinsi gani ya kutoa motisha kwa Madaktari wetu bingwa wa magonjwa ya akina mama kuwafanyia matibabu haya bure badala ya kulipia, lakini nawashakuru sana CCBRT.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, changamoto katika sekta ya afya ukiacha vifaa tiba, sasa hivi pameibuka changamoto kubwa mpya, ambao wananchi wanakuwa wakilipa bima zao za afya, wanakwenda katika hospitali, wanaandikiwa tu dawa lakini wanashindwa kupatiwa pale. Kwa hiyo, nilitaka nijue ipi ni kauli ya Serikali kwa wananchi ambao wamelipia bima zao lakini hawapati matibabu katika hospitali husika?
shimiwa Spika, ningependa kujibu swali la Mheshimiwa Silinde kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mwananchi yeyote ambaye ana kadi ya Bima ya Afya anatakiwa kupata huduma zote za afya bure ikiwemo vipimo. Nikiri kwamba katika baadhi ya vituo vya afya vya umma, hasa nadhani unazungumzia CHF tuna changamoto ya upatikanaji wa dawa zote katika vituo vyetu, ndiyo maana Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya una maduka ya dawa ambapo kama umeiokosa ile dawa katika hospitali husika unatakiwa kwenda katika duka la dawa ambalo limetambuliwa na NHIF.
Mheshimiwa Spika, kwa CHF kidogo hapo niseme kuna changamoto. Kwenye mikoa ambapo tumeenda kwenye Bima ya Afya iliyoboreshwa wao wanaweza wakapata dawa katika maduka ya dawa, kwa hiyo tunaifanyia kazi changamoto hii.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Sambamba na Sheria ya Ndoa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliridhia Sera ya Wazee tangu mwaka 2003. Ni lini Serikali italeta sheria kamili ya wazee ili waweze kutambuliwa katika nchi yetu?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli
kwamba tunayo Sera ya Wazee na sasa hivi tayari tumeshapeleka kwenye Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri
mapendekezo ya kutengeneza Sheria ya Wazee ili kuhakikisha kwamba yale ambayo tumeyaweka katika Sera ya Wazee basi yanapewa nguvu ya kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ni lini? Ni mara tu baada ya kumaliza taratibu za kutengeneza Sheria hiyo katika
Baraza la Mawaziri tutaleta Bungeni tukiwa tayari.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nimeridhika, lakini nina maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni nchi iliyoridhia Mikataba ya Kimataifa ya Haki na Ustawi wa Mtoto. Kuna
Mkataba wa Convention of the Right of the Child (CRC) wa mwaka 1989 na pia kuna mkataba wa Itifaki ya Nyongeza wa Afrika kuhusu Haki na Ustawi wa Mtoto (African Charter of the Rights and Welfare of the Child) wa mwaka 1990.
Mikataba yote hii inatutaka nchi wanachama kuhakikisha kwamba watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi wanapatiwa maisha bora na haki zao za msingi za kuishi kwa mujibu wa mikataba hii.
Je, ongezeko hili la watoto wa mitaani katika nchi yetu, ni jibu tosha kwamba Tanzania imeshindwa kuifanyia
kazi mikataba hii? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, sheria za nchi yetu, Sheria Na. 15 ya mwaka 1984 Ibara ya (6) inasema; “Kila
mtu anayo haki ya kuishi na kupata hifadhi kutoka kwa jamii kwa maisha yake kwa mujibu wa sheria.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria za nchi yetu zinakataza, Sheria za Kazi; Ajira kwa Watoto. Jamii inayopelekea wimbi kubwa la watoto wa mtaani ni kwamba imewasusa watoto, wazazi wameshindwa kuwahudumia
watoto na Serikali inakataza ajira kwa watoto. Sasa watoto hawa wanafanya kazi, siyo kwamba wanapenda, bali kwa kukidhi haki ya kupata maisha yao.
Je, Serikali inatoa jibu gani la miujiza, watoto hawa waweze kuishi huku ikitambua kwamba Sheria za Kazi
zinakataza kupata ajira na huku Serikali imeshindwa kuwahudumia watoto hawa? Je, waishi kwa miujiza gani?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru
sana kaka yangu, Mheshimiwa Khatib Haji kwa maswali yake mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, je, Serikali imeshindwa kufanyia kazi mikataba hii?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haijashindwa kufanyia kazi Mikataba
ya Kimataifa inayohusu haki za watoto. Kwa taarifa tu, taarifa zetu zote ambazo tunaziwasilisha kwenye Kamati
inayoshughulikia masuala ya haki za watoto katika ngazi ya Umoja wa Mataifa na ngazi ya Afrika, tunapongezwa kwa kazi nzuri ambayo tunafanya katika kuhakikisha ulinzi na usalama wa mtoto ikiwemo uamuzi wa Mheshimiwa Rais kutoa elimu bure, maana yake imewezesha watoto wa kike na wa kiume kupata elimu kuliko zamani. Haki kubwa ya msingi ya mtoto katika kuendelea ni pamoja na haki ya elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu ajira kwa watoto, kwamba tuna mikakati gani? Kwa mujibu wa Sheria
ya Mtoto Na. 21 ya mwaka 2009, jukumu la kwanza la kutoa chakula, malazi na mavazi kwa mtoto ni kwa wazazi. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuwataka Maafisa Ustawi wa Jamii wote kuwafikisha katika vyombo vya sheria wazazi na walezi wote ambao hawatimizi wajibu wao wa kuwatunza na kuwalea watoto wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Mtoto imesema, pale ambapo mtoto huyo hana mlezi au mzazi, basi ni jukumu
ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa, kifungu cha 94. Sisi hapa wote ni Madiwani, tunao wajibu wa kuhakikisha Halmashauri zetu zinaweka mikakati madhubuti ya kutoa malazi, chakula, kwa watoto ambao wanaishi katika mazingira magumu. Kwa hiyo, hilo suala tutaendelea kulihamasisha na kulisisitiza kwa Serikali za Mitaa.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.
Mheshimiwa Naibu Spika, walemavu wanakabiliwa na changamoto nyingi sana na mara nyingi changamoto
hizi hubaki zinawakabili wanafamilia, ikitokea bahati mbaya familia ikawa na uwezo mdogo sana, shida huwa kubwa. Je, Serikali iko tayari kuwapa walemavu wote nchini msamaha wa matibabu kama ilivyo kwa wazee, wakiwemo watu wenye ulemavu wa ngozi ambao
matibabu yao huhitaji utaalamu wa kibingwa zaidi?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mijibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2002 inatambua makundi ambayo yanatakiwa kupata msamaha wa matibabu, ikiwemo watu wenye ulemavu wasio na uwezo, maana siyo
kila mtu mwenye ulemavu hana uwezo. Watu wenye ulemavu wasio na uwezo hao wanaweza wakapata huduma za matibabu bila malipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba kwa wazee siyo wazee wote hawana uwezo, tunao wazee humu ni Wabunge wana uwezo. Kwa hiyo, sera inasema wazee wasio na uwezo, naomba hili lieleweke wazi kwa watoa huduma wote. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Vijana wengi wanaotumia shisha, bangi, madawa ya kulevya na pombe kali kali hizi, wanatumia kutokana na kukata tamaa katika maisha; nami siamini sana katika kutunga sheria, kuwakamata na kuwaadhibu. Mfano mzuri, juzi Waziri Mkuu Serikali ilipiga marufuku utumiaji wa viroba, lakini sasa kwa taarifa ya Mheshimiwa Waziri kilevi kingine kimeanzishwa. Sasa vijana wanaanza kuvuta gundi kitu ambacho ni kibaya zaidi. (Makofi)
Sasa Je, sisi kama Taifa, Serikali kuna utaratibu gani wa kuwasaidia vijana hawa ambao wengi wamekata tamaa ili waweze kupata matumaini katika maisha na waache mambo hya bila lazima ya kutunga sheria au kuwakamata?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti nimshukuru sana Mheshimiwa Selasini kwa swali lake la nyongeza. Kubwa ambalo tunalifanya sasa hivi ili kuwaepusha vijana wa Kitanzania na matumizi ya tumbaku na vileo ni kuendelea kutoa elimu kwa jamii kupitia Luninga na redio, lakini pia tumechapisha vijarida mbalimbali ili kuonesha madhara ya tumbaku pamoja na matumizi ya pombe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, wale ambao walikuwa tayari wanatumia kwa mfano, madawa ya kulevya, tumeanza mpango wa kuongeza vituo vya kutoa dawa (Methodone). Kwa hiyo, siyo tu Dar es Salaam lakini tutaanzisha Mbeya, Arusha, Tanga, Kilimanjaro pamoja na Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kubwa ni kwamba leo ni siku ya familia, kwa hiyo, tunatoa wito kwa wazazi, walezi kutimiza wajibu wao wa msingi wa malezi bora kwa watoto wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa sababu nimepata pia fursa ya kusema leo ni Siku ya Familia Duniani. Kwa hiyo, familia bora ndiyo msingi wa maendeleo ya nchi yoyote. (Makofi)
MHE. JOSEPHINE T. CHAGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nampongeza sana na kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na ya kututia moyo wananchi wa Mkoa wa Geita, lakini nina swali moja tu la nyongeza naomba nimuulize.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, Benki ya Wanawake iko Mjini Dar es Salaam, lakini asilimia kubwa ya wanawake wanaishi vijijini. Je, Serikali ina mpango gani basi wa kuweza kupeleka Benki ya Wanawake katika Mikoa yote, ikiwepo Mkoa wangu wa Geita? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Chagula kwa maswali yake mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Benki ya Wanawake imefungua matawi mawili Dar es Salaam, lakini tuna madirisha ya kutoa huduma katika Halmashauri takribani 20.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, habari njema ambazo nataka kumfahamisha Mheshimiwa Josephine Chagula ni kwamba, tulikuwa katika misukosuko kidogo, lakini tumefanya Forensic Audit ya Benki ya Wanawake na tumeweka Bodi mpya, lakini pia tuna a very dynamic young man ambaye ndiye Mkurugenzi Mtendaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sasa hivi tuko tayari, tutaongea na wenzetu wa Hazina ili sasa watukamilishie ule mtaji ambao Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne aliuahidi ili sasa tufungue matawi katika Mikoa yote na lengo letu ni kuhakikisha wanawake wanapata mikopo yenye masharti nafuu kuliko benki nyingine. Ahsante sana.(Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kutambua uwakilishi wangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu nimekuwa nikisikia Wabunge wanalalamika na kuwatetea sana wasanii pindi wanapopata matatizo kwamba tunawatumia kwenye chaguzi lakini baada ya chaguzi hatuwasaidii. Hata hivyo, waganga wa kienyeji kwa karama niliyonayo nikiangalia humu ndani wakati wa uchaguzi wawili, watatu hamkupita kwao labda Mzee Selasini...
Na siyo Wabunge peke yake ni jamii nzima na waganga hawa baada ya chaguzi…
Sawa Mheshimiwa Spika. Waganga hawa baada ya chaguzi tunawatelekeza na kuwatumia Polisi.
e, Serikali haioni umuhimu wa kujenga chuo cha kuwasaidia waganga hata kama ni kwa elimu ndogo? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Musukuma kwa swali lake la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba nchi yetu inathamini na kuheshimu kazi za waganga wa asili na ndiyo maana tumepitisha Sera ya Waganga wa Asili na Tiba Mbadala ya 2002 lakini pia kanuni. Lengo la sera hii ni kuendeleza tiba asili na tiba mbadala kwa sababu ni kweli asilimia 60 ya Watanzania wanatumia huduma za waganga wa tiba asili na tiba mbadala.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siyo tu kujenga chuo lakini tunalo pia Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala ambalo linafanya mafunzo ya mara kwa mara kwa waganga wetu especial katika kuhifadhi dawa zao na kufanya ufumbuzi. Sasa hivi tumeweka mfumo mzuri wa kuwasajili waganga wetu, tumewateua ma-DMO wote kuwa ni wasajili wasaidizi kwa ajili waganga wetu wa asili na tunaendelea kuwaenzi kwa sababu wana mchango mkubwa sana katika kutatua huduma za afya kwa wananchi. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kumekuwa na tishio kubwa la ugonjwa wa sukari hapa nchini ambao umekuwa ukiwakumba watu wa rika mbalimbali na hatuna wataalam wa kutosha katika hospitali zetu. Vilevile hata dawa wanazopewa ikifikia hatua mgongwa wa sukari anatakiwa apate insulin dawa hizo zimekuwa zikiuzwa ghali, watu hawawezi ku-afford. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na tatizo hili?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso kuhusu upatikanaji wa dawa za kisukari na ongezeko la wagonjwa wa kisukari nchini. Ni kweli sasa hivi tunashuhudia ongezeko la wagonjwa wa kisukari lakini kwa sababu kwanza ya mfumo wa maisha ambao watu wanaishi, watu hawafanyi mazoezi, wanakula vyakula bila kuzingatia lishe lakini bila ku-check afya zao mara kwa mara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kubwa badala ya kujikita kwenye kutibu tumejikita kwenye kuzuia Watanzania wengi wasipate maradhi ya ugonjwa wa kisukari. Pale ambapo Mtanzania ana ugonjwa wa kisukari kwa mujibu wa Sera ya Afya dawa ya mgonjwa wa kisukari inatakiwa kupatikana kwa bei nafuu. Kwa hiyo, tunawaelekeza Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya wanapoandaa maoteo ya dawa basi wahakikishe pia wana-order dawa za kutosha kwa ajili ya wagonjwa wa kisukari. Kama hawawezi ku-order za kutosha sisi hatuwezi kuwapelekea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili la uhaba wa Madaktari wa Meno, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri na hata wakati wa bajeti ya Mheshimiwa Waziri wa Utumishi alitoa maelezo kwamba Mheshimiwa Rais ameridhia kuajiri watumishi wa Serikali takriban 52,000 na kati ya hao tunategemea kupata watumishi wa sekta ya afya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Savelina Mwijage tutakapopata kibali tutawapanga pia kwa ajili ya hospitali za Mkoa za Kagera. Ahsante sana.
MHE. SAVELINA S. MWIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa matatizo ya Kibondo ya Madaktari wa meno ni sawasawa na matatizo ya Wilaya ya Bukoba Vijijini ya Izimbya - Katekana hawana Daktari wa meno hata mmoja wakipata tatizo la ugonjwa mpaka waende Bukoba Mjini na ni mbali sana kutoka pale kwenda Bukoba Mjini. Ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuwaletea Madaktari wa meno wa kuwasaidia hao watu wa Bukoba Vijijini?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso kuhusu upatikanaji wa dawa za kisukari na ongezeko la wagonjwa wa kisukari nchini. Ni kweli sasa hivi tunashuhudia ongezeko la wagonjwa wa kisukari lakini kwa sababu kwanza ya mfumo wa maisha ambao watu wanaishi, watu hawafanyi mazoezi, wanakula vyakula bila kuzingatia lishe lakini bila ku-check afya zao mara kwa mara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kubwa badala ya kujikita kwenye kutibu tumejikita kwenye kuzuia Watanzania wengi wasipate maradhi ya ugonjwa wa kisukari. Pale ambapo Mtanzania ana ugonjwa wa kisukari kwa mujibu wa Sera ya Afya dawa ya mgonjwa wa kisukari inatakiwa kupatikana kwa bei nafuu. Kwa hiyo, tunawaelekeza Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya wanapoandaa maoteo ya dawa basi wahakikishe pia wana-order dawa za kutosha kwa ajili ya wagonjwa wa kisukari. Kama hawawezi ku-order za kutosha sisi hatuwezi kuwapelekea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili la uhaba wa Madaktari wa Meno, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri na hata wakati wa bajeti ya Mheshimiwa Waziri wa Utumishi alitoa maelezo kwamba Mheshimiwa Rais ameridhia kuajiri watumishi wa Serikali takriban 52,000 na kati ya hao tunategemea kupata watumishi wa sekta ya afya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Savelina Mwijage tutakapopata kibali tutawapanga pia kwa ajili ya hospitali za Mkoa za Kagera. Ahsante sana.
MHE. KHADIJA NASSIR ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na malalamiko mengi kwenye Halmashauri zetu juu ya uhaba au ukosefu wa dawa lakini taarifa za Naibu Waziri hapa anasema kwamba dawa zipo. Sasa nilikuwa naomba tu Mheshimiwa Naibu Waziri atupe maelezo juu ya hili kwa kina zaidi. Ahsante.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona nisimame kwa sababu Naibu Waziri ametoa majibu mazuri sana lakini bado mdogo wangu Mheshimiwa Khadija Nassir anauliza swali kuhusu upatikanaji wa dawa. Kwa hiyo, nataka kidogo nitoe uelewa, tunapima vipi upatikanaji wa dawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapima upatikanaji wa dawa, dawa ziko zaidi ya elfu mbili, elfu tatu, elfu nne, lakini katika ngazi ya MSD tumechagua dawa 135 muhimu zaidi kwa mujibu wa Mwongozo wa WHO kwamba hizo ndiyo dawa muhimu zaidi ambazo zinatakiwa kuwepo muda wote katika ngazi ya MSD katika nchi. Kwa hiyo, kama alivyosema Naibu Waziri, MSD kati ya hizo aina 135 za dawa, tuna zaidi ya asilimia 82. Kwa hiyo, Mkurugenzi wa Halmashauri au DMO anapoomba aina 100 za dawa atapata angalau aina 82 za dawa mara moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili ya kupima upatikanaji wa dawa, katika zile dawa 135 tumechagua aina 30 za dawa ambazo tunaita life serving medicines, za malaria, maambukizi ya bakteria, HIV, dawa za akina mama wajawazito na kila kitu. Kwa hiyo, ndiyo maana Naibu Waziri sasa hivi na mimi ambavyo tunaenda kwenye vituo tunamuuliza Mganga Mkuu wa Wilaya katika zile tracer medicine 30 leo mgonjwa akiumwa ziko aina ngapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo taarifa ya TAMISEMI, anachosema Naibu Waziri ni sahihi. Mikoa hii imeonesha kwamba sasa hivi hali ya upatikanaji wa dawa katika mikoa na katika vituo ni zaidi ya asilimia 80 mpaka 90. Kwa hiyo, huo ndiyo ufafanuzi na ndiyo ukweli…

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka kutoa changamoto moja, dawa hazipatikani bure, wananchi wanatakiwa kuchangia kupata dawa. Kwa hiyo, lazima pia tuwahimize watu wakate bima za afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuko vizuri na nataka kurudia, hata NGOs kama SIKIKA ambazo zilikuwa zinatuandikia taarifa mbaya kuhusu hali ya upatikanaji wa dawa wametoa taarifa na kuthibitisha dawa ni zaidi ya asilimia 80. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Jarida la Kimataifa la Famasia limethibitisha hali ya upatikanaji wa dawa muhimu Tanzania ni zaidi ya asilimia 80. Kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuwekeza kwenye upatikanaji wa dawa nchini Tanzania. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kutokana na umuhimu wa taulo hizi za kike kwa wanawake na watoto wa kike Tanzania na kutokana na ughali wake ambao unapeleka wanawake wengi na watoto wa kike kushindwa kumudu kuzitumia na kwa kuwa Serikali imekiri kwamba maombi haya yameshawasilishwa na wadau wengi.
Mheshimiwa Spika, sasa Serikali inaweza ikatuambia nini wanawake wa Tanzania kwamba watoto wengi wanapata shida hasa watoto wa vijijini kwa sababu wanashindwa kuzipata hizi taulo kwa ughali wake. Sasa Serikali inaweza ikatuambia ni lini tutegemee kwamba lini huu mchakato utakamilika?
Mheshimiwa Spika, ingekuwa ni vizuri wakatuambia ni lini mchakato huu utakamilika kwa sababu kweli hili jambo ni suala nyeti sana kwa wanawake na watoto wa kike Tanzania? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, na mimi kwa kweli namshukuru sana Mheshimiwa Stella Ikupa kwa swali lake zuri la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, mimi ni mwanamke lakini pia nina watoto wa kike wawili, kwa hiyo, nakubaliana na yeye kabisa kwamba tuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa taulo za kike hasa kwa watoto walio vijijini na tunazo taarifa kuna watoto wanaweka mpaka majini ili kuweza kujisitiri pale wanapokwenda shule, lakini pia kuna watoto wanakosa hadi siku tano za masomo kwa sababu hawana zana za kujisitiri ili waweze kufanya masomo yao bila shida. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwahiyo, Wizara yangu nimeshamuandika Waziri wa Fedha kumuomba aharakishe mchakato huu, nilikuwa namtimizama hayupo lakini naamini wenzetu wa Wizara ya Fedha wanalifanyia kazi na tutakuja na majibu mazuri kadri itakavyokamilika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa swali la nyongeza, ninalo moja tu.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Njombe haina Hospitali ya Wilaya na ina kituo kimoja kikubwa sana cha afya ambacho wananchi wengi wanatibiwa pale na kituo hiki kipo umbali wa takribani kilometa 80 kutoka Njombe mjini mpaka kule Lupembe.
Je, Serikali haioni kama inaweza ikatoa au ikafungua duka la dawa pale Lupembe ili iwe rahisi kwa wananchi kupata dawa kuliko kusafiri umbali mrefu pale dawa zinapokosekana kwenda Kibena ambapo inatarajiwa kufunguliwa duka la dawa lakini bado halijafunguliwa? Ahsante.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, suala la kufungua maduka ya dawa, tumelirudisha kwa Halmashauri husika kwa sababu moja ya vyanzo vikubwa vya mapato katika hospitali ni kutoka mauzo ya dawa. Kwa hiyo, suala hili ni Halmashauri yenyewe ya Njombe kuweka fedha kidogo kwa ajili ya kufungua au kuanzisha duka la dawa.
Mheshimiwa Spika, sisi tupo tayari kumsaidia kupitia MSD endapo wataweka miundombinu ya kuanzisha duka la dawa tupo tayari kuwakopesha dawa zenye thamani mpaka ya shilingi milioni 50 ili wananchi wa Halmashauri ya Njombe waweze kupata dawa bila changamoto zozote, ahsante.
MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, ahsante, hapa tunachokisema ni katika nchi ambayo kuna upungufu mkubwa wa dawa, lakini vilevile unaona kuna dawa ambazo zinaharibika na tunatumia mabilioni ya fedha kuteketeza hizo dawa. Mheshimiwa Waziri wa Afya hawezi akafikiri kwamba kuna umuhimu wa kutizama kwamba inawezekana kuna ufisadi kati ya MSD na viwanda vikubwa vya dawa kugeuza nchi yetu kama dumping space ya dawa, atuletee kuja kututhibitishia hapa Bungeni kwamba hakuna ufisadi kati ya wanaonunua dawa katika nchi hii na viwanda vikubwa? Nikwambie Waziri sikurupuki, hebu tufanye hiyo kazi uone kama hujakuta kuna shida hapo. (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza nataka kumsahihisha Waziri Kivuli jambo moja, hakuna upungufu mkubwa wa dawa Tanzania na kati ya jambo kubwa ambalo Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli amelifanya ikiwemo katika Jimbo lako ni kuongeza bajeti ya dawa.
Mheshimiwa Spika, na dawa muhimu zaidi na Mheshimiwa Dkt. Mollel unajua, tunaposema upatikanaji wa dawa tunapima dawa 135 na katika Halmashauri yako ya Siha zipo. Nataka kuonesha mfano kwa sababu swali hili lilikuwa ni la Njombe, Njombe walikuwa na bajeti ya dawa shilingi milioni 43 kwa sababu ya jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, bajeti ya dawa ya Njombe ni zaidi ya shilingi milioni 150 kutoka shilingi milioni 43. Kwa hiyo, tusikariri taarifa zilizopitwa na wakati. Kama mnataka kumtendea haki Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, mtendeeni haki kwa kumpima ni kiasi gani amewekeza katika upatikanaji wa dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo la pili; Mheshimiwa Dkt. Mollel wewe ni mtaalam, kuna international standard za dawa kuchina, dawa ambazo zinaruhusiwa ku-expire. Kama umenunua dawa za milioni 100 zisifike asilimia tano ya kiasi cha milioni 100. Tanzania dawa zinazochina ni asilimia 1.8, tupo chini ya kiwango cha kimataifa cha asilimia tano. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa nini dawa zinachina Tanzania? Tunazo changamoto na namshukuru sana Mheshimiwa Jafo, kuna tatizo kubwa la maoteo. Watu hawaleti mahitaji halisi ya dawa lakini Mheshimiwa Jafo amechukua hatua na sasa hivi TAMISEMI wanajipanga kuleta maoteo halisi ya dawa.
Mheshimiwa Spika, hatua kubwa ambayo tumechukua, kwa nini dawa zinachina ni dawa za misaada. Unakuta sisi tumenunua dawa kwa ajili ya kutibu malaria unaletewa tena dawa za misaada. Tumechukua mwongozo, sasa hivi hatupokei dawa ya msaada ambayo either imekaribia kuharibika muda au dawa hiyo tayari tunayo katika bohari ya dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, niliona nimpe shule Mheshimiwa Dkt. Mollel kwa sababu yeye ni mtaalam. (Makofi/Vigelegele)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ahsante pia Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri uliyonipa. Kwanza naipongeza Serikali kwa ujenzi wa daraja la Kigamboni ambalo litatusaidia sana wananchi wa Kigamboni kiuchumi, kiutamaduni na kijamii vilevile. Naipongeza sana Serikali kwa uamuzi wake huo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa naomba niulize swali langu la nyongeza. Kwa kuwa matatizo ya Jimbo la Kigamboni kuhusiana na Mahakama ya Mwanzo yanafanana na yale ya Jimbo la Temeke na Mbagala. Mahakama ya Mwanzo ya Temeke ina hali mbaya sana, ni ya muda ina miaka zaidi ya 50 hakuna matengenezo yoyote. Pia Mahakama ya Mwanzo ya Mbagala, Magomeni na ile ya Buguruni zina hali mbaya sana. Lini sasa Serikali italeta mpango wa muda mfupi wa kuziboresha Mahakama zote ambazo nimezitaja hapa kwa sasa Mahakama hizi ziko katikati ya mji na hali ya majengo yale yanatia aibu, hayafanani na hadhi ya Jiji la Dar es Salaam?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, napenda kumthibitishia Mheshimiwa Mbunge kwamba wasubiri wiki mbili zinazokuja Wizara ya Katiba na Sheria itawasilisha mbele ya Bunge lako Tukufu bajeti ya mwaka 2016/2017 ambapo itaainisha ujenzi wa Mahakama za Mwanzo zitakazojengwa katika Kata mbalimbali na Mahakama za Wilaya katika Wilaya mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, niseme jambo moja, katika upande wa Mahakama za Mwanzo tunao upungufu wa asilimia 52 maana yake kuna Kata ambazo ni sawa na asilimia 52 hazina Mahakama za Mwanzo na kwa upande wa Mahakama za Wilaya ni karibia asilimia 81. Hata hivyo, nyie ni mashahidi, Mheshimiwa Rais ametoa shilingi bilioni 12.3 kwa Mahakama kwa ajili ya kujenga miundombinu ya Mahakama. Ukiangalia trend ya fedha, kwa mara ya kwanza Mahakama imepokea fedha za maendeleo kwa asilimia mia moja kwa mwaka huu wa 2015/2016. Kwa hiyo, tutajenga Mahakama zote kadri ya mpango wa ujenzi wa Mahakama utakavyoainishwa katika bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na maelezo mazuri sana ya Mheshimiwa Waziri, lakini Serikali imekuwa ikiahidi kwamba itajenga Mahakama za Mwanzo kwa muda mrefu sana. Chikawe one aliahidi, akaja Chikawe two, mama Nagu, Kairuki, ahadi ni ile ile. Sasa ningependa kujua Mahakama ya Nyamikoma, Kata ya Iseni, Jimbo la Sumve Wilaya ya Kwimba itakuwa lini kwenye mpango wa kujengwa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ni kweli, nakubaliana na mawazo ya Mheshimiwa Mbunge kwamba tangu Mheshimiwa mama Nagu, Chikawe na Asha-Rose Migiro tumekuwa tukizungumzia suala la ujenzi wa Mahakama za Mwanzo ikiwemo Mahakama ya Mwanzo ya Sumve.
Mheshimiwa Spika, nioneshe tu katika mwaka wa fedha 2012/2013, Mahakama ilipokea takribani asilimia 51 ya fedha kwa ajili ya maendeleo, mwaka 2013/2014 asilimia 18, mwaka 2014/2015 asilimia 7.5, mwaka 2015/2016 asilimia 100. Kwa hiyo, hoja ninayotaka kuijenga hapa chini ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli tutatekeleza mipango ya maendeleo kama tulivyoainisha katika program ya ujenzi wa Mahakama ikiwemo Mahakama za Mwanzo. Kwa hiyo, hili jambo linawezekana, nataka kumthibitishia Mheshimiwa Ndassa kwamba tutamaliza kuijenga Mahakama ya Mwanzo ya Sumve kama tulivyoahidi kabla ya mwaka wa bajeti wa 2016/2017 haujakamilika.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa katika uanzishwaji wa Benki hii ya Wanawake wa Tanzania, Wabunge wengi hususan Wanawake wakati ule walichangia mtaji ama fedha katika benki hii. Hata hivyo, Wabunge hao na wengine sasa hivi siyo Wabunge tena, hawajapewa hata shukrani hata ya kutambulika tu, hata shukurani hawajapewa. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri, Wabunge hao wa wakati ule watapatiwa lini barua hiyo ya utambulisho na hata kupatiwa hisa zao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa katika majibu yake Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kuwa uadilifu hapa hapana na kwamba wanataka kuteua tena Watendaji ama Maafisa mbalimbali ambao watakuwa waadilifu, ndiyo sasa imedhihirika kwamba, watendaji wa hii benki hawana uadilifu watendaji wake ndiyo maana ikafikia hapa ilipofikia. Je, uongozi na watumishi hao ambao si waadilifu wamechukuliwa hatua gani za kisheria? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO, Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Dada yangu Mheshimiwa Faida Bakar kwa kazi nzuri sana ya kufuatilia masuala ya uwezeshaji wanawake kiuchumi, sio tu Zanzibar lakini pia Tanzania Bara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na swali lake la pili, hawa watumishi ambao wamekosa uadilifu wamechuliwa hatua gani. Kuanzia mwezi wa Agosti mwaka 2017 tumewapeleka katika vyombo vya usalama ikiwemo TAKUKURU na Polisi, Watumishi zaidi ya 20 akiwemo aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji Magreth Chacha, kwa kukosa uaminifu na hivyo kusababisha benki kukosa hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni benki kupata hasara, Kiswahili kidogo kimepiga chenga. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo yamefanyika ya hovyo unakuta kuna SACCOS inakopeshwa shilingi bilioni moja, tunaifuatilia hiyo SACCOS haionekani hizo fedha zimeenda kwa nani. Kwa hiyo, nataka kumhakikishia Mheshimiwa Faida kwamba tunaamini PCCB na Polisi watakamilisha uchunguzi haraka na lengo letu watumishi hawa ambao hawakuwa waaminifu waweze kwenye mbele ya vyombo vya dola na kuchukuliwa hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa nataka kumthibitishia Mheshimiwa Faida kwamba, Serikali imedhamiria kuhakikisha tunapata fedha ya kukuza mtaji wa benki, tumepewa miezi sita na BOT na nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba, Mkurugenzi mpya ambaye tumemwajiri amefanya kazi kubwa, niseme ingawa ni Benki ya Wanawake lakini tumeajiri Mkurugenzi mwanaume ambaye ndani ya miezi mitano amefanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha kwamba angalau hesabu za benki zinakaa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, lilikuwa ni suala la hisa, tunatambua mchango mkuwa sana wa Wabunge wa Bunge la Tisa ambao waliweza kununua hisa kwa ajili ya kuhakikisha mtaji wa benki unakua na moja ya jambo ambalo limekwama ni lile la BOT kwamba lazima tuweke vizuri suala la shareholders, halafu ndiyo tutawapa certificate zao za hisa. Kwa hiyo, suala hili pia tutalikamilisha ndani ya siku chache. Nakushukuru sana.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nataka nimuulize Mheshimiwa Waziri kwa kuwa benki hii ukiitazama na kwa namna ambavyo anaongea kwamba inaelekea kupata hasara ni kwamba benki hii inaweza ikafa na Serikali ilikwishaahidi kuinusuru kwa kuipatia mtaji. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo ya kuipatia mtaji ili benki hiyo iweze kufanya kazi?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya sharti ambalo tulipewa na Serikali, nikiimanisha Waziri wa Fedha ni kwamba tufanye forensic audit ambayo tuliifanya mwaka jana na hiyo actually ndiyo imetusaidia tukabaini upungufu ambao ulionekana, kwa hiyo na Waziri wa Fedha anatusikiliza. Naamini kwa sababu tumeshafanya forensic audit, tumeteua Bodi mpya ya Benki lakini pia tumeweka Menejimenti mpya, kwa hiyo naamini Waziri wa Fedha atatimiza ahadi ya Serikali ya kuipatia mtaji benki kama walivyoahidi mwaka 2010.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimthibitishie tu Mheshimiwa Dkt. Kikwembe kwamba licha ya kuwa tunategemea kupata fedha kutoka Serikalini, lakini tayari tumeanza mazungumzo na Benki nyingine ambazo sitaki kuzitaja ziko tayari kufanya partnership na Benki ya Wanawake ili tuhakikishe kwamba huduma za Tanzania Women Bank zinatolewa pia katika Benki hiyo, kwa hiyo, tunakwenda vizuri na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii pia iko tayari kuhakikisha inawezekeza katika Benki ya Wanawake, kwa sababu hii ni Benki ya wote na wanufaika wakubwa wa benki hii ni wanawake. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kituo cha Kulelea Wazee Bukumbi Mkoani Mwanza kinakabiliwa na changamoto ya kukosa uzio na hivyo kuhatarisha usalama wa Wazee hawa ambao tunawapenda sana. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka mkakati kwa ajili ya kuweka uzio katika vituo vyote hapa nchini Tanzania ambapo pia ni vichache vya hawa Wazee ili kuhakikisha usalama wa wazee hawa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua changamoto ya Makazi ya Wazee ya Bukumbi na makazi mengine kama ya Mwanzagi ambayo nayo yamekuwa na changamoto kama hiyo. Tunaendelea kutenga fedha kwa awamu na nimuahidi Mheshimiwa Mbunge tu kwamba, katika mwaka huu wa fedha tutatenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa kituo cha Bukumbi.
MHE. KITETO Z. KOSHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Serikali; kwa kuwa fedha za basket fund pamoja na mambo mengine kutumika pia kupunguza vifo vya mama na mtoto. Hata hivyo fedha hizi zimekuwa zikienda taratibu na pia zina chelewa sana kufika. Kwa mfano the first quarter kwenda kuanzia Julai - Septemba zinaenda Desemba tena mwishoni kabisa na baadhi ya vituo kutokupata kwa mfano Kituo cha Ihelele kilichopo Misungwi pamoja na Hospitali ya Bukumbi hazija pata kabisa fedha.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kifedha tofauti na mfuko wa Basket Fund ambao unatolewa na wafadhili kuhakikisha kwamba vifo vya mama na mtoto vina pungua? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tunashukuru Mheshimiwa Waziri wa Afya alifika Mkoa wa Mwanza na akatembelea katika Kituo cha Karume na kuangalia kazi iliyofanyika katika Kituo cha Karume kwa pesa ambazo zimetolewa na Serikali, lakini pia Mheshimiwa Waziri alihaidi kukipatia fedha kituo cha afya kilichopo Buzuruga fedha kwa ajili ya kutengeneza theater ambapo kwa sasa kituo kile hakitoi huduma za upasuaji na kituo ambacho kinategemewa sana.
Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi hiyo ili kuendelea kupunguza vifo vya mama na mtoto katika Mkoa wa Mwanza?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Kiteto Koshuma kwa kupigana kiume na kike katika kuimarisha afya ya uzazi na mtoto ikiwemo wasichana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza kwamba fedha za Basket Fund zina chelewa nini mkakati wa Serikali katika kutafuta fedha za ndani. Kwanza kuhusu fedha za Basket Fund tumefanya mashauriano na wadau ambao wanachangia mfuko wa afya wa pamoja. Moja ya makubaliano ambayo tumeyafanya na Waziri wa Fedha akiwemo ni kwamba fedha hizi sasa watajitahidi kuzitoa kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika bajeti yetu ya mwaka 2017/2018 tumetenga rasilimali fedha za ndani kwa ajili ya kuimarisha huduma za uzazi ikiwemo kuhakikisha uzazi salama. Kwa mfano katika huduma za uzazi wa mpango kwa mara ya kwanza tumetenga bilioni 14 na zimetoka, fedha za ndani kwa ajili ya huduma za uzazi. Lakini tumetenga fedha pia kwa ajili ya kujenga maabara za damu katika mikoa mitano na tumetenga fedha pia kwa ajilia ya kujenga vyumba vya upasuaji katika vituo vya afya. Kwa hiyo sambamba na fedha za Basket Fund lakini pia tunazo hela za ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, kuhusu Kituo cha Afya cha Buzuruga, ni kweli tumepata fedha za Basket Fund bilioni 15.5 na tunategemea pia kupata fedha kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya kuboresha vituo vya afya ili kuviwezesha kutoa huduma za uzazi za dharura.
Nitumie fursa hii kuelekeza tena fedha hizi sio za kujenga mabwalo ya kulia chakula, si fedha za kujenga ukuta sifedha za kujenga mambo ambayo hayahusiani moja kwa moja na huduma za afya ya mama na mtoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua vituo vya afya vina changamoto nyingi lakini hebu tujikite katika kumuokoa mama mjamzito na mtoto mchanga baadae tutakuja kujenga wodi za kufunga vidonda lakini kwetu sasa hivi hicho sio kipaumbele, nakushukuru sana.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize swali dogo la nyongeza. Pamoja na Serikali kufanya jitihada kubwa katika kuhimiza ujenzi wa Vituo vya Afya, kumetokea tatizo kubwa sasa hivi ambalo linakabili vituo ambavyo vimekwisha; ni upungufu wa watoa dawa za usingizi. Kwa hiyo, nataka nijue tu, kwa kuwa Vituo vya Afya vingi vitajengwa katika nchi yetu, Serikali
imejipangaje?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Mwamoto kwa swali lake zuri. Ni kweli tunategemea mpaka mwisho wa mwezi Desemba, takriban Vituo vya Afya 100 vitaweza kufanya upasuaji wa dharura wa kumtoa mtoto tumboni. Kwa hiyo, tayari tumeshaongea na Chuo Kikuu cha KCMC kwa ajili ya kuendelea kutoa kozi mahususi za wataalam wa usingizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika muda huu pia, wale ambao wako tayari katika maeneo ya kazi, tumeandaa mpango wa kuweza kupewa mafunzo ya haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe tahadhari, wataalam wangu wanasema tusifanye mafunzo ya haraka, matokeo yake badala ya kuwaokoa akinamama wajawazito tukawaua. Kwa hiyo, tuna-negotiate muda wa mafunzo haya uwe angalau miezi 9 au 12. Wataalam wamekataa muda usiwe chini ya miezi sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo suala tunalifanyia kazi na naamini Mheshimiwa Waziri wa Utumishi yuko hapa, kwa hiyo, pia atatusaidia katika kuajiri wataalam hawa wa usingizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. MUSSA B. MBAROUK: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. La kwanza kwa kuwa kuna tatizo kubwa la watoto kuzaliwa na vichwa vikubwa au vichwa kujaa maji. Je, Mheshimiwa Waziri anaweza kuniambia tatizo hili Serikali inalishughulikia vipi?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Serikali inamudu kutoa dawa bure kwa wale watu wenye VVU au watu wenye TB; je, kwa nini isichukue jukumu la kuwatibu watoto hawa ambao wanaozaliwa na vichwa vikubwa ili kuondoa mateso yale ya maradhi ya vichwa vikubwa lakini pia kuondoa simanzi kwa wazazi. Kwa nini Serikali isichukue jukumu la kutoa huduma hiyo bure kwa magonjwa hao? Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, suala la watoto wenye vichwa vikubwa Serikali imechukua hatua gani. Jambo kubwa ambalo Wizara na Serikali inaendelea kulifanya ni kuhakikisha na kuendelea kuhimiza akinamama wajawazito kuhudhuria kliniki kama inavyoshauriwa na Daktari.
Mheshimiwa Spika, hii ni kwa sababu tatizo la watoto wenye vichwa vikubwa pamoja na mgongo wazi tunaweza kulitatua endapo mama ataweza pia kuongezewa dawa kwa mfano tunasema fefo dawa za folic acid ambapo nimeelekeza ziwepo katika vituo vyote vya kutolea huduma na nafurahi kusema kwamba sasa hivi ukienda kwenye zahanati ukienda kwenye kituo cha afya utakuta dawa zote za fefo zinapatikana.
Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Mbunge atusaidie kuhimiza wanawake kuhudhuria kliniki. Kwa mujibu wa takwimu ni asilimia 24 tu ya wanawake Tanzania wajawazito wanahudhuria kliniki ndani ya wiki 12 baada ya kujigundua wajawazito. Kwa hiyo pale ambapo kuna matatizo yanaweza yasionekane.
Mheshimiwa Spika, swali la pili ni suala la tunawasaidia vipi watoto wenye vichwa vikubwa na hili naomba nilibebe na Serikali ipo tayari kugharimia gharama zote za matibabu kwa watoto wote wenye vichwa vikubwa na tumeanza katika Taasisi yetu ya MOI tunafanya upasuaji bila malipo kwa watoto wote wenye vichwa vikubwa.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitoe rai kwa wanawake wenzangu wasiwafiche watoto wenye vichwa vikubwa, bali waende katika vituo na hospitali za Serikali ili tuweze kuwasaidia na kuwapa huduma. Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru. (Makofi)
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa mwenyekiti, nakushukuru sana pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri nilitaka kujua tu kwamba sasahivi wananchi wengi wameshaelimika kuhusiana na masuala ya UKIMWI. Lakini nilitaka Serikali ituambie ni kwa nini hawaruhusu watu wajipime wenyewe kwa rapid ya HIV test kwa sababu wakienda vituo vya afya usiku vinakuwa vimefungwa na kuna watu wanapenda kufanya hilo jambo kwa chap chap.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini wasiruhusiwe wapate hivi vipimo waweze kujipima ili waende kwenye hiyo shughuli wakijua wako salama au hawako salama?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya UKIMWI, upimaji unafanyika katika kituo cha afya. Lakini tumeanza mchakato ndani ya Serikali ya kufanya mabadiliko ya Sheria ya UKIMWI ili sasa watu waweze kujipima wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachotaka kumeibuka mjadala kuna wengine wanasema mtu akijipima mwenyewe atakuwa frustrated ataenda kuambukiza wengine. Kwa hiyo, tunaweka kwamba tutaanza ajipime mwenyewe mbele ya mtoa huduma za afya. Hayo ndiyo mapendekezo ambayo tumeyatoa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na tutakuja Bungeni tuwaombe Waheshimiwa Wabunge watuunge mkono, ahsante sana.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna tatizo kubwa sana la watoto njiti lakini vile vile na watoto wanaozaliwa kwa maumbile. Tofauti hii ni kwa sababu labda wakina mama hawaendi hospitali kwa wakati. Hivi karibuni majuzi majuzi tu hapa kule Kyaka kuna watoto wamezaliwa wameungana.
Sasa nilikuwa naomba kujua kama Serikali ina taarifa hii na kama inayo wanachukua hatua gani ili kuwasaidia waweze kufanyiwa labda matibabu ya haraka ili isije ikatokea kama Ndugu zetu Marehemu Consolata na Maria? Ahsante.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Susan Lyimo kwa swali lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tayari Serikali kupitia Wizara ya Afya inayo taarifa ya kuzaliwa kwa watoto wapacha ambao wameungana na tayari tumeshatoa maelekezo kwa Mganga Mkuu wa Serikali kufanya mawasiliano na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kagera kuhakikisha watoto wale wanafikishwa Muhimbili haraka iwezekanavyo ili tuweze kufanya taratibu za kuwatenganisha kadri madaktari watakavyoshauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Naibu Waziri angejibu swali hili, lakini nimesimama hapa kutoa rai kwa Watanzania wote, pale ambapo anazaliwa mtoto mwenye maumbile angalau labda ni tofauti na ilivyozoeleka, wawalete Hospitali yetu ya Taifa Muhimbili haraka iwezekanavyo ili tuweze sasa kuhakikisha Madaktari wetu Bingwa wanawapa msaada ikiwemo kuwatenganisha.
Kwa hiyo, tunaangalia kama tutawatenganisha ndani ya nchi au tutawapeleka nje ya nchi. Kwa hiyo nimesimama hapa kutoa rai tusiwafiche watoto hawa, tuwapate mapema. Mtoto yeyote ambaye tunamuona yuko na maumbile tofauti wawasiliane na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya ili tuhakikishe tunaokoa maisha ya watoto wetu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kigoma ni mkoa ambao huduma za afya zipo chini sana. Katika mikoa mitano ambayo huduma za afya ziko chini ni pamoja na Mkoa wa Kigoma.
Sasa ningependa kumuuliza Waziri, ni kwa nini Mkoa wa Kigoma haupewi kipaumbele (priority) ikiwa hali ya akina mama na vifo vya watoto ni kubwa sana? Hata ambulance tu kwenye Hospitali ya Wilaya hatuna, naomba commitment ya Wizara.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza si kweli kwamba Mkoa wa Kigoma haupewi kipaumbele katika utoaji wa huduma za afya. Hata hivyo ni kweli kwamba Mkoa wa Kigoma ni mmojawapo ya mikoa ambayo yaani viashiria vya afya hasa afya ya mama na mtoto ni mbaya, iko duni. Kwa hiyo, Serikali ina mpango tunaita result based finance (lipa malipo kwa ufanisi). Kwa hiyo Mkoa wa Kigoma ni moja ya mikoa nane ambayo tunaipatia fedha mahsusi kila zahanati, kila kituo cha afya, kila hospitali Kigoma tunaipa fedha kwa ajili ya kuhakikisha akina mama na watoto wajawazito wanapata huduma bora. Tanga haipati, Dodoma haipati na Rukwa haipati. Kwa hiyo, utakavyoona Kigoma tunaipendelea, I mean siyo tunaipendelea tunaipa kipaumbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumegawa magari ya wagonjwa sita katika Mkoa wa Kigoma, hatukugawa katika mikoa mingine. Kwa hiyo, nachotaka kumuomba Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Nsanzugwanko unafanya kazi nzuri Kasulu endelea kushirikiana na Wizara ya Afya na Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Serikali kwa ujumla katika kuimarisha huduma za afya ikiwemo afya ya mama na mtoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mengine ni masuala ya uelewa/attitude. Ameongea Naibu Waziri, wanawake kuhudhuria kliniki wanajivuta. Kwa nini wanawake wa Kilimanjaro wengi wanahudhuria kliniki na si wanawake wa Kigoma? Kwa hiyo, tumeona tunakuja na kampeni ya kitaifa tunaita Jiongeze Tuwavushe Salama; ataizindua Mama Samia Suluhu Hassan. Tunataka wanawake wa Kigoma wajiongeze kwenda kliniki kabla ya kuanza kulaumu mambo mengine. Wakijiongeza na sisi Serikali tutajiongeza tutawapa 25,000 kila mama anayejifungulia I mean Kituo cha Afya kitalipwa 25,000 kwa kila mama anayejifungulia katika Kituo cha Afya cha Kigoma. Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kukushukuru.
(Makofi)
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mpango wa maendeleo ya vitu, kwa mgano, ujenzi wa shule, visima na kadhalika ni watoto pacha na mpango wa uzazi. Serikali inasema nini katika kuhakikisha haiishii kutenga fedha bali fedha zionekane zikipelekwa eneo hilo la uzazi wa mpango?
Swali la pili, mimba za utotoni ni janga la Taifa, Mkoa wangu wa Katavi tunaongoza kwa maana ya asilimia 45. Serikali inasema nini katika kushirikiana na wananchi wa Mkoa wa Katavi ili kuwanusuru wananchi wale na janga hili?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Kapufi kwamba upo uhusiano wa moja kwa moja wa maendeleo na ongezeko la idadi ya watu na Serikali imeliona suala hili na ndiyo maana pia katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, suala la uzazi wa mpango na namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango amekuwa kisisitiza huduma za uzazi wa mpango na ndiyo maana ukiangalia tumetoka asilimia 27 mwaka 2012 sasa hivi ni asilimia 32. Kwa hiyo fedha zinatoka za Serikali na tumeamua kabisa kutumia fedha zetu za ndani badala ya kutumia fedha za wadau wa maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni mimba za utotoni, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba ni changamoto. Asilimia 27 ya watoto wa kike wamepata ujauzito kabla hawajatimiza umri wa miaka 18, kwa hiyo, katika mpango wetu wa kuzuia mimba za utotoni especially katika Mikoa ya Katavi tumeamua kutumia njia za kuwaelimisha wasichana wajizuie kuingia katika vitendo vya ngono mpaka pale watakapofikisha umri wa miaka 18.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwa kweli hali siyo nzuri, watoto wetu wa kike wanaanza ngono, asilimia 14 ya watoto wakike wanaanza ngono kabla hawajafikisha umri wa miaka 15 na watoto wa kiume ni asilimia tisa. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge mtusaidie katika kuhamasisha na kuelimisha wasichana hasa kujizuia kufanya mapenzi kabla hawajatimiza umri wa utu uzima. Ahsante.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, nina swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa uzazi salama haujafanikiwa ipasavyo kwani kunakuwepo na upungufu mkubwa wa Madaktari, wauguzi na wakunga katika vituo vingi vya afya hasa huko vijijini.
Serikali ituambie ina mpango gani mkakati wa ziada kuhakikisha kwamba mnapeleka madaktari, wakunga na wauguzi katika vituo vya afya na zahanati katika maeneo ya vijijini zaidi ili kuokoa maisha ya akina mama?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli suala la uzazi salama linategemea kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa rasilimali watu wenye sifa na ujuzi, lakini asilimia 64 kwa mujibu wa utafiti wetu sasa hivi ya wanawake wanajifungua katika vituo vya afya na wanahudumiwa na wataalam wenye ujuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nakiri kwamba zipo changamoto, Mheshimiwa Jafo ameeleza pale Serikali itaajiri watumishi wa afya 6,000 kupitia TAMISEMI na watumishi wa afya 2,000 kupitia Wizara ya afya, lakini tumeenda mbali zaidi, tumepata fedha bilioni moja, tunasomesha watumishi wa afya 200 katika kutoa huduma za dawa za usingizi na tutawapeleka katika vituo vya afya ambavyo vinaboreshwa ili sasa pale ambapo wanawake watafanyiwa upasuaji kwa ajili ya huduma za dharura watapata huduma ambazo ni salama lakini pia zinazofikika kwa wanawake wengi zaidi.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwanza nichukue nafasi hii kushukuru Serikali kwa kujenga vituo vya afya katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu. Lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa ziara yake pamoja na muda huu wa mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani amejitahidi kwenda Mbulu na kuona changamoto zilizopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Halmashauri ya Mji wa Mbulu ina Tarafa tatu; Tarafa ya Nambis katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu haina hata kituo kimoja cha afya. Changamoto kubwa inayowakabili wakina mama wa Tarafa ya Nambis katika hali ya kupata huduma ya uzazi salama. Je, ni lini sasa Serikali itatupa fedha na ahadi ya Mheshimiwa Waziri ya kwenda kwenye ile Tarafa ya Nambis ambako wananchi wengi na hasa akina mama wanapata tatizo kwenye uzazi?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Issaay kwa kazi nzuri anayoifanya kwa wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini kwa kweli kazi yako inaonekana na imetukuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la kupata kituo cha afya katika Kata ambayo haina Kituo cha afya tumeshirikiana na wenzetu wa TAMISEMI tayari kuna mpango wa kuhakikisha kwamba kata ambazo hazina vituo vya afya zinakuwa na vituo vya afya na vijiji ambavyo havina zahanati vinakuwa na zahanati.
Mheshimiwa Menyekiti, lakini naomba nitumie Bunge lako tukufu kutoa angalizo, sera ya afya inasema kituo cha afya kila kata na zahanati kila kijiji, lakini tunafanya mapitio ya sera ya afya. Tutatoa vigezo kwamba kituo cha afya kila Kata kwa kuzingatia jiografia ya eneo husika, idadi ya watu na burden of disease (aina ya magonjwa ambayo yanapatikana katika eneo hili) kwa sababu sasa hivi barabara nzuri lakini pia kuna mawasiliano ya simu.
Kwa hiyo, sitaki kuwadanganya Wabunge kwamba tutakuwa na vituo vya afya kila kata, haitawezekana. Tutaweka vigezo ili tuone ni kata zipi ambazo zitakuwa na vituo vya afya.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa swali la nyongeza.
Naomba tu kuuliza; kwa kuwa uzazi wa mpango ni moja ya mkakati madhubuti kabisa wa kuzuia vifo vya mama na watoto na nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwamba kwa mpango ujao Mkoa wa Mwanza ni moja ya Mikoa iliyowekewa mikakati, lakini Wilaya ya Nyamagana ni moja ya Wilaya zinazoongoza kwa vifo hivi vya Mama na mototo kwenye Mkoa wa Mwanza. Ni nini sasa mkakati madhubuti kwa ajili ya Nyamagana ili kuhakikisha vifo vya Mama na mototo vinakwisha kabisa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Mabula na hasa ukiona wanaume wanazungumzia suala la uzazi wa mpango maana yake tunatoka. Tutaongeza idadi ya wanawake wanaotumia njia za kisasa za uzazi wa mpango lakini nampongeza kwa kazi nzuri Nyamagana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleza tusipochukua hatua madhubuti, mwaka 2030 Tanzania itakuwa na watu milioni 70 na haiendani na ukuaji wa uchumi na itakapofika 2050 tutakuwa na Watanzania milioni 100 ambapo hatuoni pia ikilingana na ongezeko la uchumi. Kwa hiyo, tumeamua kuja na mkakati wa kuhimiza wanawake hasa walio kwenye ndoa, naomba niliseme hili, wanawake walio kwenye ndoa hutumia huduma za uzazi wa mpango na asilimia 39 ya wanawake walio kwenye ndoa wameeleza kwamba wanapenda kuchelewa kupata watoto kwa kipindi cha miaka miwili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nirudie, kwa Mheshimiwa Mabula tunaanzisha vituo vya kutoa huduma za uzazi wa mpango katika miji kwa sababu suala la uzazi wa mpango siyo ugonjwa. Wanawake wa Dar es Salaam, wanawake wa Nyamagana hawataki kwenda hospitali kupanga foleni kwa ajili ya kupata huduma. Kwa hiyo, tutawafuata akina mama ambao wanauza mboga mboga…
…tutakuwa na mobile clinic. Kwa hiyo, mama akitaka huduma anapata palebadala ya kupanga foleni masaa mawili, masaa matatu na tunawashukuru sana wadau wetu wa maendeleo ambao wametusaidia kuhakikisha huduma hizi za uzazi wa mpango Mijini pamoja na Nyamagana zinapatikana kwa urahisi.
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mkoa wa Manyara ni mkoa mkubwa tu na una wilaya tano na majimbo saba na haiwezekani kuwapeleka wazee wote katika kituo kimoja tu kinachopatikana Magugu. Je, ni nini juhudi za Serikali katika kuhakikisha Wilaya ya Hanang’, Simanjiro, Kiteto na Mbulu tunapata kituo kingine cha wazee? Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA,WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Ester Mahawe kwa kufuatilia maendeleo ya Manyara na Babati Mjini. Kwanza kwa mujibu wa Sera ya Wazee tunahamasisha wazee walelewe katika familia. Kwa hiyo Serikali haina mpango wa kujenga makazi ya wazee zaidi ya makao ya wazee 17 ambayo tunayo.
Mheshimiwa Spika, tunakusudia kutunga Sheria ya Wazee ambayo itatoa wajibu kwa watoto kutoa matunzo kwa wazee wao. Kwa sababu katika yale makambi kuna wazee wana watoto wao, wametelekezwa na familia zao. Kwa hiyo nitoe wito, niwausie Watanzania wazee hawa, wazazi wetu, wametulea, wamepigania nchi na sisi ni wajibu wetu kuwalea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha na niwaambie hata Wabunge tukichukua mzee mmoja au wawili tukakaa nao kwenye familia zetu ni baraka kwa Mwenyezi Mungu. (Makofi)
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kupata nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hali ya maambukizi katika Jiji la Dodoma inaongezeka kwa kasi sana; na kwa kuwa katika baadhi ya nchi nyingine duniani wanatumia njia mbadala mbali na damu, wanatumia mate kuweza kutambua wale waathirika wa VVU. Naomba Serikali ituambie ina mkakati gani wa ziada wa kuwatambua wale waliopata athari hii ya VVU kwa njia ya kutumia mate na hasa tukianzia na Mkoa huu wa Dodoma?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masoud, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mkoa wa Dodoma maambukizi yamepanda kutoka asilimia 2.4 hadi asilimia 5, sawa na Mikoa ya Tanga na Mwanza. Kwa hiyo, tunafanya utafiti maalum wa kuangalia kwa nini katika baadhi ya mikoa maambukizi ya UKIMWI yamepanda mwaka 2012 mpaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la njia mbalimbali za kupima, ni kweli tumekuwa na changamoto ya kuwapata watu kupima hasa wanaume na tumeona njia ambayo itaweza kusaidia wanaume kupima UKIMWI ni njia ya mtu kujipima mwenyewe. Jana tulikuwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu na moja ya kifaa ambacho tutakitumia; lakini sheria kidogo zinatukwaza, inasema kipimo cha kujipima mwenyewe haiwezekani. Kwa hiyo, tumemuandikia Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili aweze sasa kuleta mabadiliko madogo ya sheria iweze sasa kuruhusiwa kwa mtu kujipima ikiwemo kwa kutumia kipimo cha mate ambapo ndani ya dakika 15 utaweza kujua kama una maambukizi ya UKIMWI au hapana. Tunaamini mtu akishajipima mwenyewe na kujiona kwamba ana maambukizi itakuwa ni kichocheo cha kwenda katika kituo cha afya ili aweze kuthibitika na hivyo tumuingize katika mpango wa dawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai, kama alivyosema Naibu Waziri, dawa za HIV zipo kwa asilimia 100, changamoto yetu watu wapime. UKIMWI si tena sentensi ya kifo, ukiwa na UKIMWI ukipima tunakuingiza mara moja kwenye mpango wa dawa unaishi maisha safi na salama bila changamoto zozote. Ahsante sana.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru swali la nyongeza la kwanza, ni ukweli kwamba idadi ya akinamama wanaoendelea kujifungua kulingana na takwimu inaendelea kuongezeka, lile jengo kusema ukweli bado ni finyu sana kiasi cha kupelekea akinababa kushindwa kuandama na wenza wao, kinyume na alivyosema Naibu Waziri. Sasa swali langu sio kweli kwamba jengo lile haliwezi kubadilishwa, jengo linaweza likaondolewa likajengwa ghorofa angalau moja au likajengwa ghorofa moja sehemu nyingine Serikali ipo tayari kutenga bajeti kwa ajili ya kujenga eneo angalau la ghorofa moja kuweza kuwa-accommodate watu hawa ambao wanabanana kwenye corridor?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kujifungua ni tendo la faragha sana, wote mtajua Madaktari akinamama wanavyoenda kwenye hicho kitendo wengine wanaweza kutoka vinyesi, wengine wanapata kifafa cha mimba, wengine wanatokwa na maneno ya ajabu na shida nyingine kama hizo ambao wamepitia uzazi wanajua, ni kwa nini Serikali haioni umuhimu wa kutengeneza vyumba ambavyo concrete au ku-separate vile vitanda na concrete au kujenga partition ambazo mwanamke mmoja na mwingine hawawezi kuonana tofauti na ilivyo leo kwamba mmeweka pazia ambazo kiukweli wanaonana na inadhalilisha utu wao. Naomba sasa Serikali ituambie ni lini ipo tayari kutengeneza partition kwa ajili ya kustiri utu wa mwanamke pale anapokwenda kujifungua.
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSI NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia. Kwanza suala kwa nini tusiongeze jengo lingine Muhimbili Mheshimiwa Mbunge alitakiwa kutushukuru kwa sababu lile ni jengo la ziada, baada ya Mheshimiwa Rais mara tu baada ya kuapishwa alikuta mrundikano wa wangojwa akatunyang’anya ofisi Wizara ya Afya na jengo lile tukaliboresha na kuwa ni jengo la Wazazi.

Mheshimiwa Spika, nashukuru umenipa fursa ya kujibu hili swali. Muhimbili National Hospital, tumefuta kliniki za mama na mtoto katika Hospitali za Rufaa za Mikoa na Muhimbili. Pale tunapeleka wajawazito ambao wana matatizo ya kujifungua. Kwa hiyo hata ule mrundikano wa wagonjwa wataenda Mwananyamala, wataenda Amana, wataenda kwenye vituo vya afya 350 ambavyo Serikali imeviboresha ili kuviwezesha kutoa huduma. Nitoe wito kwa wanawake, Muhimbili ni National Hospital sio mtu yoyote unaenda tu kwa ajili ya chek up.

Mheshimiwa Spika, suala la pili anataka partition, Mheshimiwa Mbunge angetembelea vituo vya afya tunavyojenga, asingeuliza hili swali, tunajenga kwa kuhakikisha tumeweka partition kwa vituo vya afya vyote. Lengo letu sisi anachosema ufaragha, tunafikiria iliwezekana hata baba amsindikize mama anapotaka kwenda kujifungua. Kwa hiyo tumeliona kama Wizara na tumeweka partition zenye staha katika vituo vya afya.
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali lakini pia naomba nipongeze Serikali wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais mwaka jana mwezi wa kumi Mkoa wa Katavi Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana Mheshimiwa Ummy aliweza kukagua Hospitali tunayojenga ya Mkoa na kuongeza fedha za ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningependa kupata majibu ya Serikali je, ni lini tena ujenzi wa Hospitali yetu ya Mkoa wataongeza fedha ili kuweza kuikamilisha kwa wakati na huduma ziweze kupatikana kwa wananchi wa Mkoa wa Katavi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ili kuipunguzia mzigo Hospitali yetu ya Mkoa ambayo inajengwa na kwa msingi tunahitaji Ujenzi wa Vituo vya Afya viongezeke kwa maeneo ya mbali ili kusogeza huduma kwa wananchi wetu hususani Kata ya Ugala ambayo ni km 80 kutoka Mpanda Mjini.

Je, ni lini Serikali tena itatuongezea fedha ili tuweze kufanya ujenzi wa Kituo cha Afya kwenye Kata ya Ugala? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mbogo Mbunge wa Nsimbo, swali la kwanza ni lini tutakamilisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa!

Mheshimiwa Naibu Spika, nimthibitishie Mheshimiwa Mbogo lakini na Wabunge wote wa kutoka Katavi mwezi huu tumeongeza shilingi bilioni nukta moja kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Katavi na timu yangu ilikuwa kule Katavi Mpanda na ni matarajio yetu kabla ya mwezi wa sita tutakuwa tumemaliza Jengo la OPD, Jengo la Maternity pamoja na maabara ili tuweze kutoa huduma kwa wakazi wa Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu ujenzi wa Kituo cha Afya ni Sera yetu ya Afya kuhakikisha kwamba tunajenga Vituo vya Afya, Zahanati na Hospitali za Halmashauri. Lakini tunataka kubadilisha kidogo Sera, Sera ya Afya ambayo tunaiandika sasa hivi tunasema Serikali itajenga Miundombinu ya kutoa huduma za Afya katika ngazi zote kwa kuzingatia vigezo vikubwa vitatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kigezo cha kwanza Jiografia ya eneo husika, kigezo cha pili, idadi ya watu na kigezo cha tatu ni mzigo wa magonjwa katika eneo husika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbogo nakubaliana na wewe Kituo cha Afya kwa sababu eneo lako liko mbali na Kituo cha Afya ambacho kipo kwa hiyo tutakuweka katika vipaumbele vyetu kuhakikisha tunajenga Kituo cha Afya kwa kushirikiana na wenzetu wa Ofisi ya Rais TAMISEMI. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza:

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila binadamu ni maiti mtarajiwa, inauma sana kuona maiti inalipiwa na kama mtu hajapata hela ya kulipia maiti yake maiti ile ndiyo haizikwi na familia. Mimi naona bora Serikali ingebadilisha huu mfumo naomba sana na Bunge hili naomba mnikubalie kwa sababu iletwe hapa tukubali Wabunge iondolewe hii na Serikali kwa sababu jamani maiti ni maiti ina heshima zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa je ikiwa yule mtu maskini hahehoi anatoka kijijini maiti yake hakuweza kuilipia, kila zikiongezeka siku ile bili inaongezeka, kama mtu hakuweza kuilipia ile maiti Serikali inapeleka wapi ile maiti, inamzika kwa heshima zote au inafanya nini, nataka kujua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Faida Bakar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli wote tunathamini maiti lakini naomba niweke wazi ndiyo maana nimesimama. Hatulipii maiti kimsingi kitu ambacho tumekifanya kwenye hospitali zetu tunampokea mgonjwa tuhakikishe anapata matibabu, iwe ana pesa au hana fedha. Nitoe mfano, kama mgonjwa amelazwa ICU kwa siku ni 500,000 huduma za dawa muhimu na hiyo ni Muhimbili, lakini tukiangalia hospitali za private ICU kwa siku ni 2,500,000. Kwa hiyo, tunachofanya ni kulipia gharama ambazo mgonjwa alipatiwa siyo maiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri ameliweka vizuri.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Ahaa ndiyo ukweli! mgonjwa amepewa huduma…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, tutulie. Kama kuna tatizo kwenye hilo baadae mumuone Mheshimiwa Waziri ili mliweke sawa. Mheshimiwa Ummy.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hatudai maiti, tunadai gharama ambazo mgonjwa amepatiwa huduma. Mheshimiwa Naibu Waziri ameeleza upo utaratibu kuna Ofisi za Ustawi wa Jamii katika hospitali zetu, Mimi na Naibu Waziri tumeshasamehe wagonjwa takribani wengi tu ambao wanashindwa kulipia maiti. Kwa hiyo, badala ya Waheshimiwa Wabunge kulalamika tuwahimize wananchi wetu wakate Bima za Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kutoa mfano wote tumeona kwenye mitandao, Mama anashangilia Mume amerudi nyumbani kwa sababu ametoka kwa nyumba ndogo, matarumbeta ni shilingi ngapi ambayo amekodi? wamenunua madera sare, wameweka mishkaki, gharama pale ni kama 300,000. Toto Afya Card Bima ya Afya ya mtoto ni Shilingi 50,400, halafu mtu leo analalamika sina fedha nisaidiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuondoke katika….. kama kweli tunataka kupata huduma bora za afya, lazima wananchi wawe tayari kujiunga na Mifuko ya Bima ya Afya. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza:

Kwa kuwa watoto wengi sana wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya kikatili na wamekuwa wakiathirika kisaikolojia. Ni kwa nini Serikali sasa isiwe na mpango maalum wa kuanzisha haya madawati katika shule, kwa sababu watoto wanavyofanyiwa vitendo vya kikatili wanashindwa kwenda katika madawati huko mtaani? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Ritta Kabati kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya katika masuala ya kupambana na vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto ikiwemo kwa wananchi wa Iringa, ninaamini wanawake wa Iringa watamrudisha Bungeni ili aendelee kuwasemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tumeona kwamba watoto wengi wako katika shule zetu, shule za msingi na shule za sekondari, kwa hiyo kama Wizara tayari tumemuandikia Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Jafo ili sasa tumemuelekeza kwamba katika kila shule ya msingi na sekondari ya Serikali na shule Binafsi kuanzishwe madawati ya ulinzi na usalama wa watoto katika maeneo ya shule ili pale mtoto ambapo amefanyiwa vitendo vya ukatili kwa sababu pia wazazi hatuna muda majumbani, kwa hiyo, angalau pale akiwepo katika mazingira ya shule mtoto ataweza kujua kwamba anaenda katika sehemu gani na ni Mwalimu gani na katika muda gani naweza kueleza matatizo yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumewaelekeza Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Kata zote wawe pia wanatembelea shule hizi na Maafisa Ustawi wa Jamii mara kwa mara kwa ajili ya kutoa elimu lakini kuwasikiliza watoto ambao wanafanyiwa vitendo hivi vya ukatili. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ritta ninaahidi tu kwamba tayari tumeanza kufanyia kazi na tunaendelea na majadiliano na wadau wetu ili angalau tuanze katika Mikoa ambayo vitendo vya ukatili dhidi ya watoto ni vingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua na wewe masuala haya huwa yanakugusa kwa karibu zaidi. (Makofi)
MHE. MAULID S. MTULIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

(i) Hospitali yetu ya rufaa ya Mwananyamala ni miongoni mwa hospitali inayotoa huduma kwa wagonjwa wengi sana. Kiasi kwamba kwa siku moja inahudumiwa wangonjwa takribani 2000. Na idadi ya madaktari wetu si zaidi ya madaktari ambao wanajigawa katika shift tatu. Je, Serikali ina mpango gani kuongeza Watumishi Manesi, Wakunga na madaktari ili hospitali yetu iweze kutoa huduma bora zaidi?

(ii) Kwa kuwa hospitali yetu ya Mwananyamala imezungungwa na baadhi ya kata ambazo hazina hata zahanati, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni ametoa pesa zaidi ya milioni 90 ili kujenga zahanati katika Kata ya Makumbusho. Je, Serikali ina waahidi nini wananchi wa Kata ya Makumbusho kuongeza ili ile zahanati ile iweze kukamika kwa haraka?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli nimpongeze sana Mheshimiwa Maulid Mtulia, kwa jinsi anavyofuatilia upatikanaji wa huduma za Afya kwa wananchi wa Kinondoni, hakika Kinondoni imepata Mbunge wa Chama cha Mapinduzi ambaye anajua kufuatilia changamoto zinazowakumba wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ni lini tutaongeza watumishi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwananyamala nakubaliana na Mbunge hata ukiangalia tu takwimu za wagonjwa ambao wanahudumiwa katika Hospitali zetu za Rufaa za Mikoa ishirini na nane, Mwananyamala inaona wagonjwa kwa mwaka takribani laki tatu. Ukilinganisha na Mount Meru inaona wagonjwa elfu ishirini na nne kwa mwaka, Manyara wagonjwa elfu ishirini na saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge haja ya kuongeza madaktari wauguzi na wataalamu wengine wa Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala. Nikuahidi tu Mheshimiwa Mbunge tunafanya mchanganuo wa hali halisi ya watumishi wa Afya katika Hospitali za Rufaa za Mikoa, Hospitali za Wilaya, Zahanati na Vituo vya Afya ili kabla ya kupata nyongeza ya watumishi tuweze kuwagawanya upya. Kwa sababu unaweza ukakuta kuna Mkoa wagonjwa wanaona ni wachache lakini wana watumishi wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hilo tayari tumelibainisha katika ngazi ya Wizara, lakini swali lake la pili kwamba kuna kata hazina Zahanati ikiwemo Kata ya Makumbusho, Mheshimiwa Mbunge tumeongea suala hili, na Ndugu yangu Mheshimiwa Jafo ambaye ni kaka yangu, ni pacha wangu katika utoaji wa huduma za Afya ngazi ya msingi yuko hapa, kwa hiyo tutalishughulikia, na tutahakikisha katika fedha ambazo tunazipata kwa ajili ya utoaji uboreshaji wa miundombinu ya huduma za afya za msingi basi tunakuletea Makumbusho ili kukuunga mkono kuweza kumaliza Zahanati ya Makumbusho.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza; pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri kwamba sasa Serikali iko tayari kutuletea mashine za CT-SCAN na MRI katika Hospitali za Mikoa, ikiwemo Mkoa wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado tuna changamoto kubwa, katika Hospitali zetu za Mkoa wa Dar es Salaam hatuna mashine za kufulia nguo, hali ambayo inasababisha tuishiwe mashuka mara kwa mara, kwa sababu mashuka yanafuliwa katika Hospitali ya Muhimbili ndiyo yaletwe Temeke, Je, Serikali ina Mpango gani sasa wa kutuletea mashine za kufulia nguo katika Hospitali zetu za Temeke, Mwananyamala na Amana. (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Mariam Kisangi hasa kwa jinsi anavyofuatilia huduma za afya hasa, afya ya mama ya mtoto kwa Wanawake wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mashine za kufua nguo kama nilivyoeleza wakati tunawasilisha Bajeti yetu, tumezipokea Hospitali za Rufaa za Mikoa kuanzia tarehe 1 Julai, 2018 na tumejipanga kama Wizara kuhakikisha tunaboresha huduma zote ikiwemo miundombinu pamoja na kufunga na kununua mashine za kufulia katika Hospitali zetu zote za Rufaa za Mikoa sambasamba na kuweka Madaktari bingwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo lini, naomba nilichukue halafu tutatoa majibu ndani ya Bunge hili, lini tutaanza kuweka vifaa hivyo lakini kama nilivyoeleza tumeshaanza kuondoa vifaa vya kuweka kwa ajili ya Hospitali zetu za Rufaa za Mikoa.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, Hospitali ya Mji wa Mbulu ni Hospitali iliyokuwa inahudumia Wilaya ya Babati, Karatu na Mbulu. Hospitali hiyo iliyojengwa toka enzi za koloni imekabiliwa na changamoto lukuki, moja ya changamoto iliyoko ni uchakavu wa gari la ambulance, na kwa kuwa Hospitali hiyo iko mpakani mwa Jimbo la Mbulu Vijijini, Jimbo la Karatu na Jimbo la Babati na Hospitali za Rufaa ni Haydom na KCMC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Mbulu inashindwa kusafirisha wagonjwa wake, kutokana na upungufu wa wataalamu na vifaa chakavu.

Je, ni lini Mheshimiwa Waziri ataisaidia Hospitali ya Mji wa Mbulu kuipatia gari la ambulance?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Issaay kwa swali lake zuri, kuhusu hali ya Hospitali ya mji wa Mbulu hasa upatikanaji wa gari la wagonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tumeagiza na yanakaribia kuingia nchini magari ya wagonjwa hamsini kwa hiyo naomba nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutahakikisha gari moja linaenda Mbulu na kwa Waheshimiwa Wabunge ambao labda mnataka pia kuomba Ambulance, tumeagiza tena ambulance hamsini, kwa hiyo tunatarajia kuwa na magari ya wagonjwa mia moja, tutayagawa katika maeneo ya vipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo nitaomba tu wenye maswali kidogo watuvumilie tutakapoleta orodha ya mgao wa Ambulance basi tutaweza kuongeza zaidi, ahsante. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza suala linalohusiana na Hospitali ya Mwananyamala juu ya CT–SCAN inafanana kabisa na suala ambalo liko Mkoa wa Mtwara hasa Hospitali ya Ndanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, itakumbukwa kwamba Serikali ilifanya Hospitali ya Ndanda kuwa Hospitali ya Rufaa ya Kanda, na Wamisionari wale wamejitahidi sasa hivi wanatoa huduma ya dialysis na huduma nyingi tu na ndiyo sehemu kubwa hasa inayotumika kama Hospitali ya Wilaya kwa sababu Hospitali ya Mkomaindo haina facilities nyingi, sasa swali langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wanafanya kazi hii na Ubia wa Serikali, Je, Serikali haioni haja ili kupunguza msongamano wa watu kupelekwa Muhimbili na Rufaa hizo kuwapelekea Hospitali ya Ndanda CT-SCAN pamoja na MRI machine?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Cecil Mwambe Mbunge wa Ndanda kwa swali lake zuri, kwanza nataka kutambua umuhimu au kazi nzuri inayofanywa na Mashirika ya Dini katika kutoa huduma za Afya na sisi Sera yetu ya Afya ya mwaka 2007 inatambua na kuthamini mchango wa Mashirika ya Dini katika utoaji wa huduma za Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sasa, je tutapeleka CT-SCAN na MRI katika Hospitali ya Rufaa ya Ndanda ni kweli Hospitali hizi tumezipandisha hadhi mwaka 2010 kuwa Hospitali za Rufaa za Mikoa. Lakini Mheshimiwa Mwambe utakubaliana na mimi, tunayo Hospitali pia ya Serikali ya Rufaa ya Mkoa Ligula.

Kwa hiyo, sasa mtuambie wana Kusini, wananchi wa Mtwara kwamba tupeleke Ligula, au tupeleke Ndanda? Lakini ambaye nasimamia moja kwa moja, Hospitali zangu za Serikali kipaumbele unajenga kwako kabla hujajenga kwako kabla hujajenga kwa mwingine. Tutaendelea kuthamini na kuheshimu mchango wa Mashirika ya Dini na ndiyo maana zaidi ya asilimia 70 ya watumishi waliokuwepo katika Hospitali hizi za Mashirika ya Dini wanalipwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, zikiwepo nyingi tutapeleka Ndanda na Ligula, lakini ukiniambia nichague, nitaanza na Ligula kwa sababu ndiko pia wananchi wengi wanaenda kupata huduma za Afya katika ngazi ya Mkoa wa Mtwara. (Makofi)
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niipongeze Serikali kwa kazi nzuri ambayo anafanya kusambaza baadhi ya mashine kwenye Hospitali mbalimbali za Rufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa kuwa wagonjwa wa ugonjwa wa Kisukari umeongezeka kwa kasi na kwa kuwa mashine za kusafirishia figo ziko sehemu chache ikiwepo Dar es Salaam, KCMC na Dodoma na wagonjwa wanapata shida sana kwenda kusubiria kusafisha figo, je Serikali sasa haioni imefikia wakati muafaka wa kuhakikisha kila Hospitali ya Rufaa kunakuwa na mashine hizo za kusafishia figo? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Kaka yangu Venance Mwamoto kwa swali zuri, Mbunge wa Kilolo, ni kweli kuna ongezeko la magonjwa yasiyo ya kuambukiza hasa wagonjwa wa Kisukari, wagonjwa wa Moyo, Saratani na kuhusu sasa tuweke huduma za dialysis za kusafisha damu katika Hospitali za Rufaa za Mkoa nakubaliana naye na habari njema tunategemea kupata mashine zaidi ya sitini kutoka Saudi Arabia, ambazo tutaziweka katika baadhi ya Hospitali za Rufaa za Mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ambayo nakabaliana nayo sasa kama Waziri ni upatikanaji wa wataalamu ambao wanatakiwa kutoa huduma hiyo, lakini tunaongea na Serikali ya Saudi Arabia ikiwezekana tuwe na mpango wa haraka wa kupeleka wataalamu katika Hospitali zao na Hospitali nyingine kwa mfano KCMC, Muhimbili, JKCI na Bugando ili tuweze kuongeza ujuzi. Mashine tutaweka, naomba niseme siyo kuanza na Hospitali zote, tutaangalia kwa mfano Katavi, hatutegemei mtu atoke Katavi mpaka Mbeya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutaangalia maeneo ambayo hayafikiki Katavi, Ruvuma, Rukwa, Lindi kwa hiyo, tumebainisha kama Hospitali tano za kuanza nazo. Labda nitoe angalizo tusisubiri mpaka muda wa kwenda kupata huduma za dialysis, yapo mambo ambayo tunaweza kufanya kama wananchi kama Watanzania, ili kuepukana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza ikiwemo kufanya mazoezi mara kwa mara kuangalia ulaji wa vyakula vyetu, lakini pia kupunguza matumizi ya tumbaku na sigara itatuepusha na magonjwa yasiyo ya kuambukiza, ahsante sana. (Makofi)
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza naipongeza Serikali kwa kutujengea hospitali za wilaya tatu katika Mkoa wa Rukwa, lakini katika hizo wilaya tatu bado wilaya moja ya Sumbawanga mjini haijapatiwa hospitali ya wilaya. Je, ni lini sasa itajengewa hospitali ya wilaya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni lini Serikali sasa itapeleka fedha za ukarabati hospitali hii ya mkoa ambayo inatumika kwa sasa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Bupe Mwakangata kwa kazi nzuri ambayo anafanya katika kufuatilia upatikanaji wa huduma za afya katika Mkoa wa Rukwa hasa huduma ya afya ya mama na mtoto naamini wanawake wa Mkoa wa Rukwa wamemuona na wameiona kazi yake nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ni lini tutajenga hospitali ya wilaya katika wilaya moja ambayo haijapata hospitali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI kama alivyoeleza tumeanza hospitali 67 mwaka huu katika bajeti ziko hospitali 28 kwa hiyo, tuombe tu uvumilivu kwa wananchi ambao hawajapata hospitali moja ya wilaya, Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ya vitendo ni Serikali ya kutekeleza kwa hiyo tutajenga hospitali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba nitoe angalizo kwa sababu pia tunataka kujenga hospitali mpya ya Mkoa wa Rukwa. Kwa hiyo, ningeomba subira tukimaliza ujenzi wa mikoa mitano mipya kutekeleza ilani hii ya uchaguzi 2015/2020. Kwa hiyo, ile hospitali ya mkoa sasa tutaikabidhi kwa hospitali ya manispaa ya Sumbawanga kama tulivyofanya kwa Shinyanga na Singida ndio tutafanya hivyo, tukimaliza hospitali mpya hizi zilizokuwa zinatumika za mikao zitakabidhiwa katika manispaa. Sasa ni lini tutapeleka fedha ya ukarabati tumepata fedha takribani shilingi bilioni 14 kutoka mfuko wa Dunia wa kupambana na UKIMWI, TB na Malaria kwa hiyo tutapeleka Mkoa wa Rukwa kwa ajili ya kuboresha huduma za magonjwa ya dharura na ajali pia kuboresha huduma za ICU wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum pamoja na huduma za mama na mtoto.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi, ugonjwa wa Kansa unakuwa kwa kasi kubwa sana na Hospitali ya Rufaa ya KCMC imekuwa ikihudumia wagonjwa hao lakini tatizo kubwa sana na kilio kikubwa cha watu wa pale KCMC ni banker kwa ajili ya kuweka mashine ya Radiotherapy kwa ajili ya mionzi ya watu wenye matatizo ya kansa. Je, ni lini sasa Serikali itatatua tatizo hilo hasa ikizingatiwa hata katika bajeti ya maendeleo mwaka huu fedha hizo hazijatengwa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Suzan Lyimo kwa swali lake la nyongeza na kwa kweli amekuwa akifuatilia suala hili la upatikanaji wa bankers kwa ajili ya utoaji wa matibabu ya mionzi, radiotherapy katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini KCMC. Ni lini watu wa Kanda ya Ziwa ni mashahidi tunaenda hatua kwa hatua. Tumeanza kuweka huduma za mionzi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa Bungando na sasa hivi karibia asilimia 95 ya wagonjwa wa Kanda ya Ziwa wanapata huduma za matibabu ya saratani chemotherapy na radiotherapy katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni lini tunaenda hatua kwa hatua tunahitaji takribani bilioni 9 na juzi nilikaa na timu yangu nikawaeleza tunaenda vizuri kwa upande wa Hospitali za Rufaa za Kanda na changamoto kubwa ya kanda ya KCMC kwa kweli nakubaliana na wewe ni bankers. Tukiweka bankers tutakuwa tumekamilisha kweli bajeti ya mwaka huu hatujaweka lakini kama unavyofahamu tunapata fedha kutoka vyanzo vingine mwenyewe pia ni mdau wa kanda ya Kaskazini. Kwa hiyo, tutahakikisha, Mheshimiwa Naibu Spika, siyo kama najipendelea lakini tutahakikisha kwamba tunaweka bankers katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini.
MHE. SELEMANI M. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza Mkoa wa Katavi ni mkoa ambao hauna hospitali ya mkoa na unategemea sana Hospitali ya Manispaa ya Mpanda kwa ajili ya kutoa huduma kiasi kwamba wagonjwa wamekuwa wengi na kuifanya ile hospitali kuzidiwa. Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka fedha kwa ajili ujenzi wa hospitali ya mkoa ili iweze kuendana na muda kwa wakati?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Moshi Kakoso kwa swali lake la nyongeza kuhusu ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Katavi. Na kama nilivyojibu katika swali la msingi kipaumbele chetu kama Serikali ni kukamilisha ujenzi wa Hospitali za Rufaa za mikoa katika mikoa mipya ikiwemo Mkoa wa Katavi. Mheshimiwa Kakoso tayari timu yangu ilishafika Katavi mwezi uliopita na hivi leo nikitoka hapa naenda ofisini kwa ajili ya kusaini mikataba ya ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Katavi. Lakini tutaanza na majengo manne ya kipaumbele, tutaanza jengo la wagonjwa wa nje OPD tumelitengea takribani shilingi bilioni 3 tutajenga jengo kwa ajili ya huduma ya uzazi na watoto wachanga martenity block tumetenga 3.3 bilion, tutaweka jengo la ICU na Theatre na jengo la nne la kipaumbele ni jengo kwa ajili ya huduma za radiolojia na mionzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwatoe hofu wananchi wa Katavi kama tulivyoahidi kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM Mheshimiwa Kakoso usiwe na shaka 2020 utasimama kifua mbele baada ya kuwa tumetekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa kujenga Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Katavi. Kwa hiyo, takribani kuna kama bilioni 9 tumezitenga kwa ajili ya Katavi mwaka huu wa fedha 2019/ 2020.
MHE. SONIA J. MAGOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri wa Afya nina maswali mawili ya nyongeza. Mahakama kuu ilitamka kuwa vifungu vya Sheria ya Ndoa ambavyo vinaruhusu ndoa za utotoni havistahili kutumika hivyo vifanyiwe marekebisho ndani ya mwaka mmoja na kuweka umri wa miaka 18 kuwa ndio umri wa chini wa mtoto kuweza kuolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Serikali kupitia Mwanasheria Mkuu ilikata rufaa juu ya shauri hilo. Je, Serikali haioni kwa kukata rufaa inaendelea kukubali athari zinazompata mtoto kiafya na pia kuondoa haki ya fursa za kimaendeleo kwa mtoto?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wanawake wengi wamekuwa wakipata shida sana pindi wanapotengana na wenza wao ama kupoteza wenza wao hasa wa vijijini na hii ni kutokana na kutokujua sheria mbalimbali na kupelekea watoto wengi kukosa haki zao za msingi kama afya, malazi, chakula na elimu.

Je, Serikali haioni kuna umuhimu wa kutoa elimu kwa wanawake hawa kuanzia ngazi ya vijiji ili kuweza kuwasaidia watoto hawa kupata elimu kuanzia ngazi ya chini?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Sonia Magogo kwa maswali yake mawili ya nyongeza. Suala la marekebisho ya Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 maelezo yalishatolewa ndani ya Bunge lako tukufu na Waziri wa Katiba na Sheria, kwa hiyo nisingependa kurudia maelezo ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa sababu suala hili sasa hivi liko chini ya Waziri wa Katiba na Sheria na yeye ameahidi ndani ya Bunge lako tukufu kwamba linafanyiwa kazi. Suala la kutoa elimu kwa kina mama na watoto ambao wanapata matatizo au changamoto au haki zao mara wanapotengana na waume zao, kwa kweli niyashukuru sana Mashirika yasiyo ya Kiserikali yamekuwa yakifanya kazi kwa karibu sana na Serikali katika kutoa elimu kwa jamii kuhusu masuala ya haki za wanawake na watoto katika ndoa na mara ambapo kunakuwa ndoa imevunjika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kama nilivyoeleza katika majibu yangu ya msingi tumepitisha Sheria ya Legal Aid Act, No. 1 ya Mwaka 2017, na lengo letu kwa kweli ni kuhakikisha sasa wanawake hasa wa vijijini wanapata huduma za msaada wa kisheria pale ambapo kunakuwa na changamoto ndani ya ndoa. Mheshimiwa Sonia nikiri kwamba tutaongeza jitihada za kuelimisha jamii katika ngazi zote hasa katika ngazi ya vijijini ili kuhakikisha kwamba wanawake wanatambua haki zao. Pia tutawaelimisha na wanaume kwa sababu mwisho wa siku ili tuweze kupata mafanikio mazuri lazima tuwaelimishe na kuwahamasisha wanaume kuheshimu na kutambua haki za wanawake na watoto ndani ya ndoa na nje ya ndoa.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kumekuwa na vitendo vingi vya unyanyasaji na hasa kwa watoto wadogo ambavyo haviripotiwi kabisa na akina mama kwa sababu ya kuogopa wakati mwingine usalama wao, lakini wengine pia kwa sababu ya kutojua haki zao za Kisheria. Sijui Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha akina mama wanapata elimu hiyo ili watoto wanapopata matatizo ya kudhalilishwa waweze kuwa na ujasiri wa kuripoti vitendo hivyo?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini kwa swali lake la nyongeza kuhusu uwepo wa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto. Swali lake kwa ujumla anasema tuna mkakati gani wa kutoa elimu, nimetoa maelezo wakati najibu swali la Mheshimiwa Sonia Magogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kubwa tutaendelea na jitihada za kutoa elimu kwa jamii kupitia vyombo vya habari hata ukiangalia TV, ukisikiliza radio na vipeperushi mbalimbali, tumekuwa tukichapisha juu ya suala hili la vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto. Mkakati mwingine Mheshimiwa Mwakasaka ambao tunautumia, tuna namba ya simu bure 116 ambayo inatoa fursa kwa mtu yeyote na nitumie fursa hii kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba mwananchi yeyote ambaye ana tatizo la vitendo vya ukatili dhidi ya watoto mnaweza mkajaribu hata sasa hivi kupiga namba 116 itapokelewa na taarifa dhidi ya vitendo hivyo inafika katika mahala, vyombo vya Serikali na kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuameanzisha Madawati ya Jinsia na Watoto katika Jeshi la Polisi. Tuna madawati zaidi ya 350 ambayo kazi yake pia ni kutaka kutoa uhuru kwa wanawake na watoto kwenda kutoa taarifa juu ya vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto bila vikwazo vyovyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema suala hili kwa kweli tutaendelea kulifanyia kazi, nikiwa kama Waziri ninahusika na masuala ya haki na ustawi wa mtoto. Kwa kweli kuna ongezeko kubwa la vitendo vya ukatili dhidi ya watoto, ubakaji na ulawiti umeendelea kuongezeka katika jitihada zetu. Kwa hiyo, tuanze sisi ndani ya familia, kwa sababu vitendo hivi vinatokea pia katika familia husika, watu wa karibu ndiyo wanajihusisha kwa kiasi kikubwa na vitendo hivi vya ukatili dhidi ya watoto.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwanza nimpongeze Waziri kwa jitihada hizi za kuelimisha jamii kuhusu unyanyasaji wa watoto, lakini ni ukweli watoto wananyanyaswa kwa kiasi kikubwa sana. Watoto wa kiume wanalawitiwa, watoto wa kike wanaingiliwa na wengine wanaingiliwa kinyume na maumbile, sasa hii inatokana na ukimya wa sisi wazazi kwa jumla.

Sasa ni lini Serikali itaanzisha mkakati wa makusudi kabisa wa kutembelea haya mashule na kukaa na wazazi ili kuwaeleza jambo hili wazazi waondoe aibu na waongee na watoto wao kwa uwazi kabisa kuhusu jambo hili? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Selasini kwa swali lake zuri la nyongeza hasa kwa kukiri kwamba jukumu la kwanza linaanza na sisi wazazi walezi. Tarehe 16 Juni, 2019 ambayo ni siku ya Mtoto wa Afrika, Serikali itazindua agenda ya Kitaifa kuhusu wajibu wa wazazi na walezi kwenye ulinzi na usalama wa mtoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ajenda hiyo lengo lake kubwa ni kutaka kwanza kuweka wajibu wa kwanza kwa mzazi mlezi kutimiza wajibu wake katika malezi, matunzo na usalama wa mtoto. Lakini kwamba pia kama alivyoeleza, hiyo ajenda pia itatuka sasa tuendelee kwenda katika shule mbalimbali za msingi na ndani ya Wizara tunafikiria katika kila shule ya msingi na Serikali kuweka dawati la ulinzi na usalama wa mtoto. Kwa sababu pale mtoto amepata tatizo angalau anajua nitakimbia kwa mwalimu fulani ambaye naweza kujieleza kwa uhuru na kwa faragha na masuala yangu yakasikilizwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe rai kwa wazazi wenzangu na mimi ni mzazi, pamoja na kazi kubwa tunayoifanya ya kutafuta shilingi lazima tutimize wajibu wetu kwa watoto wetu. Wazazi anaweza ikapita wiki mbili, wiki tatu hamuulizi hata mtoto unaendeleaje, nimekuwa nikisema kila siku. Mimi namkagua binti yangu, lazima tufanye huo utaratibu hawa watoto wa miaka mitatu, minne, mitano angalau muogeshe hata mara moja kwa wiki utajua ana changamoto gani, ana matatizo gani, lakini tukiwa busy na kutafuta fedha kwa kweli watoto wanaharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naliongea hili kwa uchungu, kuna mtoto analawitiwa miezi mitatu mzazi hajui, unajiuliza hivi huyu mtoto kweli ana wazazi na walezi. Kwa hiyo, nimshukuru sana Baba Mchungaji na tunaomba viongozi wa dini watusaidie, katika mahubiri yenu hebu tuhubiri tunaenda wapi kama kizazi, kama jamii ya Watanzania. Kwanini vitendo vya ubakaji na ulawiti dhidi ya watoto wa kike na wa kiume vinaendelea kuongezeka. Sheria peke yake hatuwezi kumaliza suala hili, lazima tutimize wajibu wetu kama wazazi na walezi kuhusu matunzo na usalama wa watoto wetu, ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOYCE B. SOKOMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Serikali kutengeneza makazi ya hawa wazee lakini nasikitika kusema makazi hayo yapo kwenye hali mbaya sana hali inayo sababisha hata maana ya kuwasaidia wazee hawa isiwepo kutokana na makazi hayo kuwa na hali mbaya sana yaani mazingira siyo rafiki ni mabovu na hili swala la wazee siyo la leo wala jana ni la siku nyingi kwa nini Serikali isione ni wakati muafaka kuwawekea makazi rafiki na yaliyo bora na salama kwa maisha binadamu?

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka Matibabu bure kwa wazee lakini nichelee kusema wazee bado wanapata shida sana ya matibabu bure na bado wapo mitaani wanazurura na kuombaomba mfano mzuri ni hapa Dodoma wazee bado wana randaranda hovyo ukizingatia Dodoma ni makao Makuu ya Serikali na ndio kioo cha Nchi yetu ya Tanzania.

Je, Serikali haioni kwamba sasa ni wakati muafaka wa kulifanyia kazi kinaga ubaga jambo hili ili kuondokana na adha hii ya kudhalilisha wazee tukikumbuka kwamba wote sisi ni wazee watarajiwa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuboresha Makazi ya wazee nchini kulingana na upatikanaji wa fedha. Hadi sasa Wizara imeboresha majengo ya makazi 3 ya Nunge-Dar es Salaam, Njoro-Kilimanjaro na Maguu- Manyara pamoja na kuunganisha makazi 4 ya Chaz - Morogoro, Mkaseka - Lindi, Nandanga - Lindi na Nge’he – Ruvuma.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika swali la Msingi, Serikali imeendelea kuweka Mikakati ya kuwahudumia Wazee Wasiojiweza nchini, hususan kuwapatia matibabu bila malipo. Kuhusu wazee wanaozurura ni kwamba wajibu wa kuwatunza wazee ni wa familia, ndugu jamaa na marafiki. Nitoe rai kwa jamii husika kuendelea kutimiza wajibu wao wa kuwatunza wazee. Aidha, Serikali itaendelea kutoa huduma za msingi kwa wazee wasiojiweza ambao hawana ndugu kupitia makazi 13 ya wazee.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo :-
Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kufahamu Mradi wa SITETEREKI ulileta mafanikio kiasi gani wa kubadili mienendo ya vijana baada ya tathmini? Naipongeza Serikali kwa kuandaa ajenda ya Kitaifa ya afya kwa vijana na uwekezaji.

Je, utaratibu upoje katika kufanikisha elimu kwa vijana wenye Ulemavu wa akili kwani ni kundi ambalo lipo katika makundi yenye hatari kubwa ya kuathirika pia?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, Mradi wa SITETEREKI ulianza 2018-2019 ambao ni mradi wa miaka mitano 2018/2023 ni jukwaa la vijana ambalo linatumika kuwafikishia ujumbe vijana kuhusu elimu ya afya ya uzazi. Jukwaa hilo, sehemu kubwa umekuwa ukifadhiliwa na USAID kupitia Mradi wa Tulonge Afya lakini kitaalamu Wizara ndio ilikuwa inatekeleza katika Mikoa 20 ya Tanzania Bara ambayo ilileta mafaniko ya kupunguza mimba za utotoni na kusimamia malengo ya kishule. Tathmini ya kati ya mradi itafanyika kuanzia mwezi Juni, 2020 na tathmini kubwa itafanyika mwaka 2023.

Mheshimiwa Spika, tumefanya rejea ya waelimisha rika (Pre Educators Manual) kwenye mapitio ya rejea hiyo tumeweka sura ya kuwafikia vijana wenye ulemavu ambapo tunategemea kuukamilisha hivi karibuni. Kwa kushirikiana na wadau wa Pathfinder na UMATI kuna Mtaala unaotengezwa ili kuwafikia vijana wenye ulemevu.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri kabla haujawa Mbunge na hatimaye Naibu Waziri tulikuwa wote Manispaa ya Kinondoni; na unafahamu kwamba tulikuwa tuna mpango wa kujenga stendi Kata mashuhuri ya Kawe yenye wananchi wengi sana. Sasa, sasa hivi umeshakuwa Naibu Waziri upo huko kwenyewe huko. Sasa naomba uniambie, kwa sababu mkakati wa Kinondoni unaujua, ni lini tutajenga Stendi ya Kawe? Kwa sababu tuna eneo la iliyokuwa Wizara ya Mifugo na eneo la Tanganyika Packers. Ni lini tutajenga stendi Kata ya Kawe? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri Dkt. Dugange kwa majibu mazuri, lakini nimshukuru Mheshimiwa Halima Mdee kwa swali lake, kwamba lini tutajenga stendi katika Kata ya Kawe.

Mheshimiwa Spika, nimesimama, tulipata maelekezo kutoka kwa Kamati yako ya Bajeti lakini pia Kamati ya Utawala na TAMISEMI kwamba tufanye mapitio ya mwongozo wa kutekeleza miradi ya kimkakati nchini, kwa sababu inavyoonekana mwongozo ule unazipendelea Halmashauri zenye mapato makubwa na kuzifanya Halmashauri zenye mapato madogo kutopata rasilimali fedha za kutekeleza miradi ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halafu fedha hizi ni grant, ukipewa hazirudi; kwa hiyo tulijadili, na sisi tumekubaliana na ushauri wa Kamati. Unamuacha Makete, unampa Kawe, Kinondoni ambaye ana mapato ya zaidi ya bilioni 30. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge, Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha tunapitia mwongozo ili halafu sasa tuweke vigezo vya jinsi ya ku-finance miradi ya kimkakati ili hata Halmashauri zisizo na fedha na mapato ya kutosha waweze kupata fedha za kutekeleza miradi ya kimkakati ikiwemo ujenzi wa stendi, masoko na vitega uchumi vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Kawe itasubiri kwa kuwa kipaumbele chetu tutaangalia uhitaji wa Halmashauri maskini au zenye mapato madogo Zaidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kwa kuwa mradi huu unaligusa pia na Jiji la Dodoma na kwa kuwa wataalam walishakaa na kuibua miradi hii kuanzia ngazi ya mtaa, kata mpaka Ofisi ya Rais, TAMISEMI: -

Je, ni lini sasa Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Wizara ya Fedha mtakaa pamoja mkwamue vikwazo vilivyopo ili wananchi waweze kunufaika na huu mradi? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru sana Naibu Waziri, Mheshimiwa Silinde kwa majibu mazuri, pia namshukuru Mheshimiwa Anthony Mavunde na mleta swali, mtani wangu Mheshimiwa Mabula kwa swali zuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, tunatambua kwamba mradi wa TACTIC ni mradi wa kimkakati katika Halmashauri za Majiji na Miji 45. Serikali ya Awamu ya Sita kama alivyosema Naibu Waziri, tumeweka mradi huu kuwa ndiyo mradi wetu wa kielelezo katika kujenga miundombinu ya barabara, masoko pamoja na madampo ya taka katika miji 45.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la Mheshimiwa Anthony Mavunde ni lini TAMISEMI tutakaa na Wizara ya Fedha? Ndiyo maana nilitaka kusimama. Jumatatu ya tarehe 10 Mei, 2021 nilikaa mimi pamoja na Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Mwigulu kwenye Ofisi ya Wizara ya Fedha pamoja na wataalam wetu na tukakubaliana kwamba majadiliano yamekamilika, sasa tunapeleka World Bank kwa ajili ya taratibu za kusaini mkataba wa kuanza ujenzi wa mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu mradi huu ni muhimu sana kwa Jiji la Mbeya, nafahamu mradi huu ni muhimu sana kwa Jiji la Arusha, nafahamu mradi hii ni muhimu sana kwa Jiji la Dodoma, pia ni muhimu sana kwa Jiji la Mwanza. Na mimi Tanga Jiji mradi huu kwangu ndiyo utanipa kura za kurudi Bungeni mwaka 2025.

Kwa hiyo, kutopatikana kwa TACTIC maana yake sitarudi Bungeni 2025. Kwa hiyo, naubeba kama mradi wangu, lakini na kwa Majiji mengine yote 45 tutahakikisha tunaanza utekelezaji mara moja. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na jitihada ambazo Serikali inafanya juu ya kuajiri walimu lakini kuna changamoto kubwa kwenye maeneo ya vijijini kukosa walimu wa kike.

Ningependa kujua mkakati wa ziada wa Serikali inafikiri nini juu kuondoa hizo changamoto ambazo watoto wa kike wanakutana nazo shuleni.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ni swali zuri na mimi kama mama tunahitaji pia kuwa na walimu wanawake katika shule zetu za msingi na sekondari ni moja ya kigezo tutaki- take into consideration katika kutoa ajira mpya lakini pia kufanya reallocation ya walimu katika shule zetu za msingi na sekondari hususani za vijijini.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hali iliyopo Halmashauri ya Mji wa Mbulu ya ukosefu wa walimu wa sayansi inafanana kabisa na hali ya Halmashauri zote za Mkoa wa Pwani kuwa na uhaba wa walimu wa sayansi.

Je, ni lini sasa Serikali itatupatia walimu hawa wa sayansi ili kuweza kukidhi mahitaji? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Naibu Waziri Mheshimiwa Silinde kwa majibu mazuri, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Hawa Mchafu kutaka kujua ni lini Serikali itapeleka walimu wa sayansi katika shule za sekondari za Mkoa wa Pwani.

Mheshimiwa Spika, kama ulivyosema, tunakiri tunayo changamoto ya uhaba wa walimu wa sayansi na uchambuzi ambao tumeufanya ndani ya miezi mitatu kuna shule takribani 1,000 za sekondari wanafunzi wetu hawajawahi kukutana na mwalimu wa physics face to face, lakini tuna shule takribani 400 watoto wetu wa sekondari hawajawahi kumuona mwalimu wa hesabu akiingia darasani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tatizo hili tumeliona na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kutupa kibali cha kuajiri walimu katika mwaka huu wa fedha wa 2020/2021. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge tunakamilisha uchambuzi wa maombi ya walimu ambao wameomba nafasi hizi za ajira tulizozitoa na kipaumbele kama tulivyosema ni kutatua changamoto hii ya walimu wa sayansi hususan pia katika masomo ya hesabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongeze, sambamba na kuendelea kuomba kibali cha ajira kutoka kwa wenzetu Ofisi ya Rais - Utumishi tumeona ipo fursa ya kutumia maendeleo ya Information Communication and Technology (ICT) ili pia kuwawezesha wanafunzi wetu kupata masomo au walimu wa sayansi na hesabu kupitia mtandao.

Kwa hiyo, hili ni jambo ambalo tumeliona, tutaweka walimu wazuri watarekodi mada zote muhimu halafu wanafunzi wetu watakuwa pia wanaweza kusoma masomo ya sayansi kwa kutumia njia ya mtandano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante Jimbo la Makete linakata 23, kata tatu hatuna shule za Sekondari na katika vipaumbele ambavyo nilivileta kwenye wizara ni Kata ya Mlondwe ndiyo ianze kujengwa shule ya Makete Boys na tuliahidiwa kupewa milioni mia 600, lakini hadi sasa milioni 600 hatujazipata.

Je, ni lini milioni 600 zitafika ili tuanze ujenzi wa Makete boys na baadaye tufuate shule Kigala na baadaye tufuate shule ya sekondari Bulongwa? Naomba majibu ya Serikali.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA
SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri Silinde kwa majibu mazuri sana kwa maswali yaliyotangulia nimesimama kuhusu swali lililoulizwa na Mheshimiwa Sanga ni lini shilingi milion 600 zitatoka kwa ajili ya kujenga sekondari katika Kata ambazo hazina sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumekamilisha orodha ya sekondari 214 za kila Jimbo ambazo zitapata shilingi milioni 600, lakini Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema atatupa shilingi milioni 470 kilichonikwamisha hatujatoa mkeka Waheshimiwa Wabunge wanabadilisha mara kwa mara. Kwa hiyo, hapa simu yangu imekufa nilikuwa nitoe taarifa na ndiyo maana nimesimama kutoa taarifa kwa Waheshimiwa Wabunge kujiridhisha na kile kipaumbele ulichoweka cha Kata yako nitatuma ujumbe kwenye group la Wabunge kusema umpigie mtu gani, uangalie je, hiyo kata yako iliyowekwa ndiyo kata ya kipaumbele. Lakini Mheshimiwa Dkt. Mwigulu yuko tayari tumekwama sisi kwa sababu Wabunge wanabadilisha badilisha.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ile shule ya Mkoa mmoja na waomba sana Waheshimiwa Wabunge tuliomba mchakato uanze kwenye RCC. Kwa hiyo, tumeandikiwa barua na Makatibu Tawala wa Mikoa, wakisema kwamba shule ile moja. Kwa hiyo, kutakuwa na 214 za kila Jimbo, halafu tutanza na moja ya kila mkoa, naomba sana Wabunge mapendekezo yametoka kwa Makatibu Tawala wa Mikoa. Kwa hiyo, tunaomba sana tumeona kuna watu wanabadilisha toa wilaya hii peleka hii sisi tumezingatia ushauri wa Makatibu Tawala wa Mikoa.

Mheshimiwa Spika, by tarehe 15 Mheshimiwa Sanga mkitupa confirmation, hela Mheshimiwa Dkt. Mwigulu yupo tayari zitakuwa zimeshaenda kwenye halmashauri zenu. (Makofi)
MHE. MARIAM M. NYOKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, naomba niulize swali langu lingine la nyongeza.

Kwa kuwa mazingira ya nje ya majengo ya hospitali hii ya Mkoa wa Ruvuma sio rafiki hasa kwa watumishi na wagonjwa kwa kipindi cha mvua; je, Serikali ina mpango gani wa kuweka paving pamoja na kujenga mifereji ya maji ya mvua katika hospitali hii?
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Mariam Madalu Nyoka kwa swali lake zuri, lakini kwa kufatilia maendeleo ya utoaji huduma katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Ruvuma.

Mheshimiwa Spika, nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kuboresha hospitali zote za rufaa za mikoa kwa kuwa ni kiungo muhimu cha utoaji huduma kati ya ngazi ya msingi na huduma za rufaa za juu. Kwa hiyo, tumepokea changamoto ya mazingira ya nje ambayo hayavutii na nikuahidi kwamba najua pia kuna suala la barabara tutawasiliana na TARURA ili pia kuweza kuweka lami katika barabara ambayo inaelekea kwenye hospitali ya rufaa ya mkoa.

Mheshimiwa Spika, suala la tent hilo ni jambo ambalo tutalifanyia kazi.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Hospitali ya Mkoa wa Simiyu haina wodi za kulaza wagonjwa, wodi ya wanaume, wanawake na watoto; je, ni lini Serikali itajenga wodi hizo?
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Esther Midimu kwa swali lake la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti yetu ya 2022/2023 tumetenga fedha kwa ajili ya kuongeza wodi za kulaza wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu na baada ya Bunge mimi mwenyewe nitakwenda Simiyu pamoja na Mheshimiwa Esther Midimu ili kuhakikisha kwamba ujenzi unaanza haraka iwezekanavyo. (Makofi)
MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza naishukuru sana Serikali kwa kazi nzuri iliyofanya kupitia fedha hizi za UVIKO na naishukuru sana Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kwenye jibu la msingi ameeleza vifaa hivi vimefika zaidi ya asilimia 94 katika Hospitali ya Tumbi; je, Mheshimiwa Waziri anatuahidi ndani ya mwezi Oktoba kwamba CT Scan itafanya kazi, yupo tayari kuwaelekeza wataalam wake kuhakikisha kweli mwezi Oktoba vifaa hivi vitafanya kazi kwa kuwa ni jambo la kihistoria na halijawahi kutokea kuwa na CT Scan ngazi ya hospitali za rufaa za mkoa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa kazi kubwa imefanywa ya ujenzi ya miundombinu ya afya ikiwemo vituo vya afya Mkwakwani tuna vituo vya afya 10 kutokana na tozo na hospitali za wilaya na zahanati.

Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kupunguza ujenzi wa miundombinu mipya ili ijielekeze kuhakikisha miundombinu hii ambayo imejengwa kwa kasi inapata vifaa tiba kwa kuwa pia inakuja na mpango wa bima ya afya ili mpango huu ukianza kutekelezeka hospitali zote na vituo vya afya viweze kuwa na vifaa tiba? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Subira Mgalu kwa maswali yake mazuri na hususan kusema kwamba suala la ununuzi wa vifaa tiba ni jambo la kihistoria ambalo limefanywa na Rais Samia Suluhu Hassan haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa CT Scan kama nilivyosema itafungwa by October, 2022 lakini kabla ya kuanza kufanya kazi lazima pia tufanye testing (tufanye majaribio) na watu wa Tume ya Atomic Energy lazima pia watoe kibali cha kuanza kutumika. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Subira Mgalu kwamba suala hili kwetu ni la kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, suala la pili kuhusu je, kwa nini sasa Serikali isijielekeze katika kuimarisha huduma za afya? Nakubaliana nawe Mheshimiwa Subira na mimi nilishatoa maelekezo kwa wenzangu Wizara ya Afya, lakini kwa Ofisi ya Rais – TAMISEMI. Tumejenga zahanati nyingi, tumejenga vituo vya afya vingi, tumejenga hospitali za wilaya nyingi. Sasa hivi tujikite kuhakikisha kwamba huduma zinatolewa zenye ubora katika hospitali tulizojenga.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kipaumbele cha Wizara ya Afya au kwa sekta ya afya sasa hivi ni mambo mawili; ubora wa huduma, kuhakikisha huduma zinapatikana, dawa zinapatikana, tunao watumishi wa kutosha lakini pamoja na lugha ambazo wataalam wetu wa afya wanawahudumia wananchi. Kwa hiyo, hiki ndiyo kipaumbele cha sekta ya afya katika kipindi hiki.

Mheshimiwa Spika, sisemi kwamba hatutajenga zahanati na vituo vya afya kwa sababu Waheshimiwa Wabunge wengi mnataka, lakini tutajikita katika maeneo ya kipaumbele ambayo tunadhani labda kuna umbali mrefu, kuna idadi kubwa ya wananchi, lakini pia mzigo wa magonjwa bado ni mkubwa katika eneo hilo husika. Nakushukuru sana.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza pamoja na majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, cyanide na mercury ni kemikali ambazo zote zina athari kubwa kwa maisha ya watumiaji. Lakini pia cyanide ndiyo ina gesi ambayo inatoa sumu kali ambayo inaweza kusababisha vifo kwa watumiaji ukilinganisha na zebaki.

Je, Serikali imetoa elimu kiasi gani kwa watumiaji wale ili kuepukana na madhara ambayo yanaweza kupelekea vifo kwa wachimbaji wadogo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa kuwa upatikanaji wa cyanide ni mchakato mkubwa na unahitaji mtaji mkubwa lakini pia unahitaji kuwa kibali ili uweze kununua cyanide jambo ambalo linapelekea wachimbaji wadogo wakashindwa kuipata hiyo kemikali ya cyanide.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha wachimbaji wadogo ili waweze kuipata kwa gharama nafuu ambapo sasa waweze kufanya shughuli zao za kila siku kama walivyokuwa wanaitumia mercury ambayo ilikuwa inaweza kukamata kwa 0.1 ambapo kwa kila siku wanakuwa wanazalisha na kuweza kupata chakula chao cha kila siku kulinganisha na cyanide? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Hassan Zidadu Kungu kwa maswali yake mawili mazuri hususan katika kuhakikisha tunawalinda wachimbaji wadogo wa madini na madhara ya matumizi ya kemikali hatarishi.

Mheshimiwa Spika, ni kweli wachimbaji wadogo huko nyuma na wengine hadi sasa wanatumia madini au mercury kwa Kiswahili zebaki ili waweze kuchenjua dhahabu ambayo wanatenganisha dhahabu, udogo na madini mengine. Lakini kimataifa nchi yetu inawajibika kusitisha matumizi ya zebaki kwa mujibu wa Mkataba wa Minamata. Kwa hiyo, ndomana saizi tunasisitiza matumizi ya cyanide.

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba cyanide ni ghali ukilinganisha na zebaki, kwa hiyo wachimbaji wengi wadogo hawana uwezo wa kumudu. Tunaendelea kushirikiana na Wizara ya Madini kuhakikisha kwamba tunatoa elimu ya matumizi ya cyanide na namna ya kujikinga na madhara na watu wa madini wako hapa.

Mheshimiwa Spika, pia tumeshajenga vituo vya mfano kwa ajili ya wachimbaji wadogo kujifunza jinsi gani ya kutumia madini haya ya cyanide kwa wachimbaji wadogo, kwa mfano pale Rwamgasa, Mkoani Geita tumeweka kituo hicho, Katente pia Mkoani Geita na Itumbi, Mkoani Mbeya.

Mheshimiwa Spika, lakini nataka nikiri bado tunayo kazi kubwa ya kufanya kwa sababu bado wachimbaji wetu wadogo hawana elimu, lakini pia vifaa kinga vya kujikinga na madhara yatokanayo na madini haya hatari ya cyanide.

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kwa kutumia mamlaka ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Wizara ya Madini pamoja na wenzetu wa OSHA kuhakikisha kwamba wachimbaji wadogo wanapata elimu pamoja na kujikinga na madhara ya madini haya.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, tatizo lililopo katika Hospitali ya Mkoa wa Lindi Sokoine ni sawa kabisa na tatizo lililopo katika Hospitali ya Mkoa wa Mtwara Ligula, kukosekana kwa Daktari wa magonjwa ya ndani pamoja na mifupa. Je, Serikali ina kauli gani kutuletea, ingawa tunajua tunayo hospitali ya Rufaa lakini hii ni kuhusu ya Mkoa?
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Nimesimama ili kuwatoa hofu Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali kwa sasa ina mpango maalum wa kusomesha Madaktari Bingwa na Madaktari Bingwa Bobezi ambapo katika Mwaka huu wa Fedha wa 2022/2023 tutasomesha Madaktari Bingwa na Bobezi 139. Madaktari Bingwa na Wabobezi 136 tutawasomesha nje ya nchi. Tumeamua kuwasomesha kwa utaratibu wa set badala ya kupeleka Daktari Bingwa Mmoja wa magonjwa ya ndani inabidi awe na Muuguzi Bingwa wa masuala ya usingizi, kuwepo na mtoa huduma Bingwa wa radiology, kwa hiyo ndiyo jambo ambalo tunaenda nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, tuna Madaktari Bingwa 457 tunawasomesha katika pair moja moja. Kwa hiyo, niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge, kwanza tutafanya assessment, tunafahamu kuna baadhi ya hospitali za Rufaa za Mikoa zinazo idadi kubwa ya Madaktari Bingwa kuliko hospitali za pembezoni. Mheshimiwa Waziri wa Utumishi, ameshanipa kibali kama wamezidi niwahamishe ili kuwapeleka ambako kuna shida wakati tukiendelea kusubiri hawa ambao tunawasomesha.

Mheshimiwa Spika, tunatambua ni changamoto kubwa lakini ndani ya miaka miwili itakuwa ni historia chini ya mpango wa Samia Suluhu Health Super Specialization Program. Ahsante sana.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pia nishukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa, mfumo huu wa kutumia dirisha la wazee unaonyesha una mapungufu makubwa. Je, Serikali haioni kuwa ipo haja sasa kubadilisha mfumo huu na ikiwezekana wazee wapewe kadi kabisa za bima ya afya, kuliko kupewa vitambulisho kama ilivyokuwa sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa wazee wengi wanaoishi vijijini hawajui kabisa kwamba kuna dirisha lile la afya, kutumia huduma za afya; je, Serikali ina mpango gani wa kuwafikia wazee hawa ili nao waweze kupata huduma hii muhimu kwao kama wazee wenzao wanaoishi mijini? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi kwa maswali yake mawili ya nyongeza hususani katika kuhakikisha kwamba wazee wetu wanapata huduma bora za matibabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba tubadilishe mfumo wa kutumia dirisha la wazee lakini tutumie mfumo wa bima ya afya kwa wote. Nitumie Bunge lako Tukufu kuwashawishi Waheshimiwa Wabunge wote, Ijumaa kupitisha Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote, kwa sababu moja ya jambo ambalo linakwenda kutatua ni kuhakikisha kwamba wazee pia wanapata huduma za matibabu bila ya kikwazo cha fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Wizara ya Afya tunaamini kwamba, kutungwa kwa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote kutaboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa wazee ikiwa ni pamoja na dawa. Kwa sababu wazee wengi sasa hivi wanakwenda kwenye dirisha la wazee, dawa hakuna, wakiwa na bima tunaamini watapata dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Wazee wa Vijijini hawapati hii huduma, tumekinyanyua kile kitengo kilichokuwa kina shughulikia huduma za wazee, kimekuwa sasa ni section, kwa hiyo, kina Mkurugenzi Msaidizi, kazi yake kila siku ni kuangalia huduma za matibabu kwa wazee, huduma za rehabilitation pamoja na huduma za palliative za shupaa. Kwa hiyo, tunaamini kabisa pia hii itaongeza muamko katika kutatua changamoto za wazee. (Makofi)
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada zinazochukuliwa na Serikali za kupunguza vifo vya wajawazito, lakini kasi ya upunguaji hairidhishi: Je, Serikali imefanya tathmini ya sababu zake?

Swali la pili; kwa kuwa vifo vingi vya wajawazito vinatokana na uzazi pingamizi na majengo mengi yaliyojengwa hususan majengo ya upasuaji hayana wataalamu na vifaa tiba: Je, Serikali inatoa tamko gani juu ya jambo hilo? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Lucy Sabu kwa suala hili kubwa na nyeti ambalo lote linatugusa wanawake, akina baba na wanaume. Kwa suala la vifo vitokanavyo na uzazi ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha tunavipunguza kadiri inavyowezekana. Sababu za vifo hivi tunazifahamu Mheshimiwa Lucy, ni pamoja na uchungu pingamizi, kutokwa na damu kabla, wakati na baada ya kujifungua. Pia kuna suala la kifafa cha mimba na kuna maambukizi pia ya bakteria.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Lucy pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan inayo mikakati mingine ya ziada ya kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi. Kuanzia Julai tutatekeleza mradi mkubwa chini ya ufadhili wa World Bank wa Shilingi bilioni 460 ambazo tunazielekeza kwenye huduma za akina mama wajawazito na watoto wachanga.

Mheshimiwa Spika, tutajenga vyumba vya wanawake wajawazito mahututi katika hospitali za wilaya, tutawajengea uwezo watumishi wa afya ili waweze kutoa huduma bora za uzazi wakati wa kujifungua, tutaweka vifaa tiba pamoja na dawa za kuzuia vifo vya akina mama wajawazito ikiwemo dawa ya oxytocin pamoja na dawa ya kuzuia kifafa cha mimba Magnesium Sulphate.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba taarifa rasmi kuhusu vifo vitokavyo na uzazi tutazipata mwezi Oktoba, 2022 baada ya Tanzania National Bureau of Statistic kukamilisha taarifa au utafiti kuhusu hali ya afya na demografia nchini Tanzania. Ndiyo tutaona vifo vinapungua kwa kasi ya aina gani. (Makofi)
MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Wizara hii kwa Mheshimiwa Ummy ameitendea haki sana kwa kufanya kazi kubwa sana; na kwa kuwa akina mama wengi wale ambao wanajifungua kwa operation wamekuwa wakilalamika kuhusu maumivu makubwa sana kutokana na zile sindano ambazo wamekuwa wakichomwa mgongoni; na kwa kuwa kuna pesa hizi Shilingi bilioni 460 za World Bank; na kwa kuwa Mheshimiwa Ummy nakuamini una wataalamu na watafiti wa kutosha: -

Je, kwa nini Serikali isifanye utafiti na kujua ni nini hasa kinachosababisha akina mama hawa wapate maumivu ambayo almost yatasababisha ulemavu mara baada ya kujifungua hapa Tanzania? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Lucy Mayenga, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Shinyanga kwa swali lake lakini kwa jinsi anavyowapambania wanawake wa Mkoa wa Shinyanga ikiwemo akina mama wajawazito.

Mheshimiwa Spika, nalipokea swali la Mheshimiwa Lucy Mayenga, ndiyo maana nimesema, Rais Samia ameruhusu mradi huu wa investing in people na focus yake ni afya ya uzazi, mama na mtoto. Fedha zote hizi tutazipeleka katika kuboresha huduma za uzazi. Kwa hiyo, hiyo sindano ambayo wanachomwa akina mama wajawazito ni dawa ya usingizi ili waweze kufanyiwa upasuaji. Tutafanya tathmini kama alivyoshauri.

Mheshimiwa Spika, pia nataka kuwaahidi, tunakwenda kuhakikisha tunatumia huduma za ubingwa za uzazi katika mradi huu ambao tunautekeleza. Vile vile tutajenga hospitali ya mama na mtoto katika Mkoa wa Dodoma ya kwanza ya Kitaifa ili kujenga uwezo wa afya ya uzazi, mama na mtoto katika nchi ya Tanzania. Kwa hiyo, suala hili tunalibeba, tutalifanyia kazi. (Makofi))
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Katika mwaka wa fedha wa 2017/2018, Serikali ilichangia ujenzi wa vituo viwili vya afya Wilaya ya Longido Mkoa wa Arusha; Kituo cha Engarinaibo na kituo kingine kilichopo mpakani mwa Namanga na Kimokoa, lakini hadi sasa vituo hivi havijakamilika: -

Je, ni nini mpango wa Serikali kuhakikisha vituo hivi vimekamilika?(Makofi)
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Catherine Magige, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Arusha kwa swali lake naye tunatambua jitihada zake anazombana katika kutatua changamoto za wanawake wa Mkoa wa Arusha ikiwemo kuimarisha huduma za mama na mtoto.

Mheshimiwa Spika, suala la vituo vya afya ambavyo havijakamilika, Wizara ya Afya inashirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa vituo vyote vya afya vilivyojengwa, pia Waheshimiwa Wabunge pamoja na kuviwekea vifaa na vifaa tiba.

Nimeshamuelekeza Katibu Mkuu wangu, anakutana na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, TAMISEMI tufanye tathmini ya vituo vya afya vyote ambavyo vimejengwa, havijakamilika na ambavyo havina vifaa.

Ninawaahidi Waheshimiwa Wabunge fedha hizi ambazo ninazitaja zinakwenda kujikita katika kuweka au kuboresha huduma katika ngazi ya msingi. Kwa sababu asilimia 80 ya wanawake wanajifungulia katika zahanati na vituo vya afya. Kwa hiyo, fedha tutazielekeza nyingi Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ajili ya kukamilisha miundombinu.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, mwaka jana mwezi Aprili ilikuwa, wakati tuko kwenye Bunge la Bajeti kama hivi, niliuliza the same question na Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel bahati nzuri naye ndiyo bado Naibu Waziri wa Afya, walinijibu mpaka mwezi wa Kumi na Moja ule upungufu wa Madaktari Bingwa 11 ambao ulikuwepo mwaka jana hospitali ya Kitete na mpaka sasa hivi bado upo, kwamba wangeweza kuwa wameweza kutupunguzia mpaka mwezi wa Novemba, 2022 bado mpaka sasa hivi.
WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu mazuri na nimshukuru sana Mheshimiwa Mwakasaka kwa swali lake kuhusu ni lini Serikali itapeleka Madaktari Bingwa katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Kitete.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana tulipata kibali cha ajira cha kuajiri Madaktari Bingwa lakini hatukuwapata sokoni, kwa hiyo mkakati tunautumia Serikali ni kama alivyoeleza Naibu Waziri ni wale ambao tayari ni Madaktari katika hospitali husika tunawapeleka kuwasomesha, na bahati mbaya hawajamaliza kusoma. Hatua ya haraka ambayo tumeifanya Mheshimiwa Mwakasaka, tumefanya tathmini ya Madaktari Bingwa tumegundua katika baadhi ya hospitali za Rufaa za Mikoa kuna Madaktari Bingwa wengi kuliko katika baadhi ya hospitali nyingine. Kwa hiyo, tunafanya re-distribution tunawatawanya upya, tumekwama tu kidogo kwenye fedha.

Mheshimiwa Spika, mwaka huu pia tumepata kibali cha ajira, tutaajiri Madaktari Bingwa na pia tutawasambaza katika Hospitali za Rufaa za Mikoa. Changamoto waliomaliza kidogo ni wagumu kuingia sokoni kwa hiyo mkakati tunaoutumia ni kuhamasisha Madaktari katika hospitali zetu za Rufaa za Mikoa wakasomee Udaktari Bingwa halafu wakirudi wabaki pale pale katika hospitali zao.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri ahsante sana kwa majibu yako. Naomba kuelewa wanasomeshwa na Serikali ama wanatiwa moyo ili wakajisomeshe wenyewe kwenye huo utaalam wa ziada.

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, ni swali zuri. Kipekee tunampongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa mara ya kwanza tumeanzisha utaratibu unaitwa Samia Suluhu Super Specialist Program tunasomesha Madaktari Bingwa zaidi ya 400 ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, tumeenda mbali hatuwasomeshi mmoja mmoja tunawasomesha katika utaratibu wa set, kama ni Daktari Bingwa kwa ajili ya upasuaji wa mifupa kwa hiyo anakwenda Daktari Bingwa Upasuaji wa Mifupa, anakwenda Nurse kwa ajili ya ICU - Intensive Care Unit, anakwenda Mtu wa Usingizi na anakwenda Mhudumu. Kwa hiyo, tunasomesha katika ngazi ya set na tunampongeza sana Rais Samia, tunayo bajeti ya kama bilioni nane na wiki ijayo tutakuja Bungeni kuomba tena bajeti Wabunge mtupitishie kwa ajili ya kusomesha Madaktari Bingwa nchini, ahsante sana.