Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mussa Azzan Zungu (31 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi, lakini kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Vilevile nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya, nitoe pongezi kwa Mawaziri wake kwa kazi nzuri sasa wanayoifanya na kuwashukuru wananchi wa Jimbo langu la Ilala kwa kunirudisha tena kwenye Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la ujangili likiendelea litapunguza mapato kwenye Taifa letu. Mimi nilikuwa naomba kutoa ushauri and I stand to be corrected.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa majangili ambao wako katika mbunga hizi, wanajichanganya na wawindaji halali, hivi Serikali ikipiga marufuku uwindaji kwa kipindi cha miezi mitatu, hakuna mtu yoyote kuingia na silaha kwenye mbuga hizi; na vyombo vya ulinzi vikafanya operation maalumu ya kusaka majangili hawa; nafikiri inaweza ikasaidia kupunguza tatizo katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri wa Maliasili na Utalii, pembe za nduvu ambazo ziko kwenye bohari, wazifanyie audit na wazifanyie DNA. Iko hatari kuwa takwimu za pembe za nduvu ziko sahihi, lakini ndovu zile ambazo ziko kwenye magodauni haya zisiwe sahihi. Inawezekana pembe nyingine wala hazitolewi kwenye mbuga, zinatolewa kwenye ma-godown haya ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri kwa taarifa yake na Mapendekezo ya Mpango wake. Ametoa taarifa Bungeni kwamba gharama za kujenga reli ya kati itafika kama bilioni saba, fedha za Kimarekani, takribani kama shilingi trilioni 15. Fedha hizi ni nyingi sana na tusijitie hofu kwa gharama kubwa kama hii ili reli hii isijengwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Zambia wamejenga reli yao kilometa 2,200 na madaraja 48, kwa one billion US Dollars. Sisemi train ya Zambia ipo sawasawa na ya kwetu, lakini naomba design cost zipatikane ili tujue gharama sahihi ya reli hii ili iweze kujengwa, iweze ku-support bandari yetu na bandari nyingine ili uchumi wa Taifa yetu uweze kukua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye Mpango, kuna Mpango wa kununua ndege. Kununua ndege na kujenga hii reli, Serikali haiwezi. Serikali ijikite kwenye mipango ya huduma za afya, elimu na kilimo. Miradi mikubwa kama hii iachiwe sekta binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta binafsi ipo tayari kufanya. Sioni kwa nini Serikali miaka yote haitaki kushirikisha sekta binafsi ikajipunguzia gharama za kutumia fedha za umma kujenga reli hii au kununua ndege hizi na badala yake ikatumia kwenye mipango mingine. Sekta binafsi ikifanya shughuli hizi, itapunguza hata tatizo la watu kula rushwa kwa fedha hizi za umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndege hizi ambazo Serikali inataka kununua; ushauri wa kwa Serikali, wasafishe vitabu vya ATC ili wakaribishe sekta binafsi iendeshe na ilete ndege nchini mwetu. Watanzania wanataka usafiri. Ukienda Marekani, hakuna Shirika la Ndege la Serikali. Sioni sababu kwa nini Serikali ijiingize kwenye miradi mikubwa na baadaye ikaingia kwenye hasara sababu ya kutokuwa na watendaji waaminifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais, kwa kuleta elimu bure Tanzania. Sasa hivi wazazi wengi sana wanapeleka watoto wao kusoma na kujiandikisha. Zipo changamoto, mwanzo ni mgumu. Fedha haziwezi kwenda kwenye shule zote kwa muda mfupi sana ambao umewekwa, lakini changamoto hizi tukiipa muda Serikali, itatafuta njia ya kuhakikisha agizo hili la Rais linatekelezwa kwa ufanisi na Watanzania wakapata win-win situation wao na Serikali yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo issue ya Watanzania kushindwa kuwa na viwanja kutokana na Serikali kutokuwa na mipango madhubuti ya ku-ring fence viwanja maalum vya watu wenye kipato cha chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Malaysia, Serikali imeweka sheria kabisa ya kuweka viwanja na madhumuni yake ni kusaidia watu wao wa kipato cha chini. Viwanja hivi vinawekewa sheria kwamba yeyote mwenye kipato cha kati, haruhusiwi kuingia kwenye viwanja hivyo. Serikali ikijenga nyumba katika viwanja hivyo, watu wenye kipato cha kawaida hawaruhusiwi kuingia au kumiliki nyumba hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano, maana yake watu kama sisi Wabunge ambao wana uwezo wa kukopa na kujenga, hawataruhusiwa kuchukua viwanja kama hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndiyo inasababisha watu kujenga kwenye mabonde. Hakuna mtu anayetaka watu wake wajenge kwenye mabonde wapate matatizo ya mafuriko, inasikitisha sana, lakini hawana njia nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeambiwa kuna mradi wa World Bank kwenye maeneo haya ya mabonde ambayo watu wanaishi. Ninachokiomba, taarifa ambazo ziko kwenye mitandao, World Bank wanataka kufanya huu mradi lakini wameweka component ya fidia. Kama hizi fedha zimefika, fidia hii ilipwe tunusuru maisha ya hawa watu. Tusiingie tu na mazoezi makubwa ya kuvunja bila kutazama na mustakabali wa wananchi hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sitetei wananchi wakae katika maji, wala msinielewe vibaya; wanataka wao waendelee kukaa katika mabonde maeneo ambayo ni hatarishi; lakini taarifa za wao kupewa viwanja Mabwepande, siyo kweli. Nalizungumza hili na ninazo takwimu. Wananchi wa Mchikichini ambao walikumbwa na mafuriko mwaka 2011 walikuwa 4,200; viwanja allocation ilitoka kwa wananchi 80 tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna taarifa kwamba Mawaziri hawa wanapewa na Mamlaka ya Mkoa kuambiwa kuna watu wanakimbia Mabwebande au wameuza Mabwepande, siyo kweli! Kama kuna mtu ameuza kiwanja chake Mwabwepande watuletee taarifa na majina ya watu waliouza na waliokimbia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie, kuna watu wako tayari kuliboresha bonde hili…
MWENYEKITI: Tunakushukuru kwa mchango wako.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana, naanza na kauli ya Waziri wa Nishati alipotoa kauli kuwa nchi nzima umeme utakuwa ni 27,000/= lakini kwa Ilala hiyo bei hakuna. Jiulize kwa nini Ilala itozwe laki tatu, laki nne, kuunganisha umeme, lakini nchi nzima mikoa yote ambayo Mwanza, Arusha, wanalipa bei ya chini zaidi ya Ilala; tatizo liko wapi na kwa nini kuna formula kama hiyo kwa kuletewa watu wa wilaya hii yetu ya Ilala? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, ada ya tozo ya fire. Tulitoa taarifa yetu ndani ya Bunge kuwa ni kubwa mno, sio kwa mjini tu maeneo yote nchini, tozo ya ada ya fire kwa majumba ya ghorofa ni zaidi ya 250,000 kwa mwaka, ni kubwa zaidi ya kodi ya majengo, kitu ambacho wananchi hawawezi. Tulikubaliana itolewe na ipunguzwe isiwe 250,000 ishuke mpaka 10,000 kwa mwaka kutokana na extraction ambazo hawa watu wa fire wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naingia kwenye mitandao ya simu. Kuna mambo mengi yanazungumzwa kwenye mitandao, kuna kashfa nyingi zinapitishwa kwenye mitandao, kuna taarifa nyingi ambazo si za ukweli ziko kwenye mitandao kuhusu gharama na ada mpya ambayo Serikali na kodi inaitaka kwenye simu nchini mwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania ina watu zaidi ya milioni 55. Walipaji kodi kwenye nchi hii hawafiki milioni tano, hawa milioni tano kwa kweli, kodi wanayolipa wao inaweza ikabeba maendeleo ya nchi hii kwa watu milioni 50? Haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima tujitoe muhanga, lazima tukubaliane na mabadiliko ya nchi yanavyokwenda. Yesu Kristu kipindi chake na kwenye kitabu alichokujanacho alisema ya Kaisari yaende kwa Kaisari na ya Mungu yaende kwa Mungu. Mtume Muhamad (SAW) na kwa waislamu alianzisha vita na mataifa ya kiarabu kwa kutokutaka kutoa zakaa. Unachukua kwa mwenye nacho unampa asiyekuwanacho. Leo wananchi wanalilia barabara, wanataka maji, wanataka elimu, wanataka bima za afya, pesa zinatoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe wananchi huu utaratibu wa kwenye mitandao wa kutoa maneno ya kashfa, kutukana viongozi, kitu ambacho mnashindwa kuelewa kila uki-post tangazo lako la matusi au tangazo la kashfa ujue unalipa kodi. Kila ukitukana, kila uki-post, elewa unalipa kodi hiyo ndio nia yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi juzi Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameweka vizuri sana kwenye miamala hii kodi hii ya simu ameweka kuanzia 10 mpaka 200. Hebu tuchukue kwa wale ambao watalipa 20 kwa siku, 20 tu ambayo ni 600 kwa mwezi kwa watu milioni 30 ni bilioni 216. Tumejaribu kupanua wigo wa kodi hata yule mwananchi wa kawaida naye awe na mchango wa barabara, awe na mchango wa bima, awe na mchango wa masuala ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unaposema vijana wengi wako katika mitandao vijana hawa wazazi wao wanataka kwenda hospitali. Vijana hawa Ndugu zao wanataka kwenda kujifungua. Vijana hawa wanataka bima kwa wote. Vijana hawa wana wazazi wao wagonjwa. Vijana msipotoshwe na taarifa ambazo zinatolewa ambazo hazina ukweli. Sasa mtu kama mimi niliyekubuhu hata nikipigwa madongo sijali, wala siogopi, sababu najua wananchi wanataka maendeleo. Maendeleo yatakuja na kodi. Isipokuwa Waziri wa Fedha, nikuombe, ada hizi za simu, kodi hii maalum ambayo Wabunge wote tumekubaliana, lazima ui-ring fence; inakwenda kwenye maji, inakwenda kwenye barabara, inakwenda kwenye bima kwa wote, isiwe pesa hii inatumika kwenye posho, isiwe pesa hii inatumika kwenye semina, isiwe pesa hii inatumika kwenye mambo ambayo hayana tija kwa … (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo Mheshimiwa Rais, Mama Samia Mama yetu, amempa kila Mbunge milioni 500 kwa jimbo. Kila shule, kila kata isiyokuwa na sekondari, nampongeza Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Waziri wa TAMISEMI, leo ametutangazia kila kata isiyokuwa na sekondari milioni 600 wanapewa. Hizi hela zitatoka wapi kama sio kodi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na tuna uwezo wa kulipa hizi kodi kwa kiwango cha kila mtu. Yule mwenye uwezo mkubwa atalipa kodi kubwa, the rich will pay more, the rich will be taxed more and taxes are collected they are not paid; kodi inachukuliwa hailipwi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, watu tujiandae na mabadiliko ya kufunga mikanda kusaidia Taifa letu liende mbele. Tuna miradi ya SGR inataka hela, tuna miradi ya bwawa la umeme la Mwalimu Nyerere linataka hela, tuna miradi mipya ambayo Serikali inataka hela kwa hiyo, lazima tulipe kodi tupate hela. Kuna barabara za vijijini, tunataka mazao ya wakulima yafike kwenye masoko kwa uhakika, kuna maeneo ambayo barabara hazipitiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wananchi wa Ilala ndio walionituma, nawazungumzia wao, najua hawa wote wanaopondaponda kwenye mitandao hawakai Ilala, wao wanakaa Kivule, Bombambili, sijui Majimatitu, sisi watu wa Ilala tunataka maendeleo. Tunataka barabara, tunataka miundombinu ya mifereji, tunataka lami kwenye majimbo yetu ya mjini tuweze kuchangia pesa za kutosha tusaidie majimbo ambayo hayana uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo Ilala tunakusanya 1,100,000,000 kwenye ada ya ku-park magari. Parking za magari kwenye Wilaya ya Ilala one billion kwa mwezi Mheshimiwa Waziri na hizi pesa wala haziji kwetu zinakwenda kusaidia maeneo mengine. Sasa tuboreshe maeneo yetu ya mjini, ili tuweze kusaidia… (Makofi)

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Zungu kuna Taarifa.

T A A R I F A

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kumpa Taarifa Mheshimiwa Zungu kwamba, kodi hii ya simu imejibu kilio cha muda mrefu cha Watanzania cha kutaka kila Mtanzania alipe kodi kwa usawa. Kwa hiyo, kodi hii ya simu Wabunge tunalipa, viongozi wakubwa wanalipa, mpaka mtu wa chini analipa kwa usawa. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Nadhani uli…

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea Taarifa. Na kulingana na matumizi yako.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hakuna mtu anaandikiwa barua, leo hakuna mtu ananunua stamp, leo hakuna mtu anakwenda posta. Leo sio lazima ukamtembelee Ndugu yako kulipa nauli ya 2,000 ya nauli ya basi, unapiga simu unazungumza naye, watu hawayaoni? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo uko Mwanza unauliza bei ya soko ya ng’ombe Pugu, huna haja ya kumtuma mtu aje Pugu unauliza kwenye simu kwa hiyo, simu hizi ni chocheo kubwa la maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naungana na Serikali kuanzisha kodi hii, isipokuwa matumizi ya pesa hizi yalindwe yasiende kutumika kwenye maeneo ambayo hayastahiki kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo Serikali ina mpango wa bima kwa wote. Wananchi wetu wanalalamika dawa hakuna, wananchi wanalalamika wanakwenda kujifungua maisha magumu, wananchi wanalalamika huduma za hospitali zinapungua. Kwa ada hii na pesa hizi ambazo tutazipata ndio kimbilio la wananchi wetu kupata maisha bora. Ndio kimbilio la uzazi salama kwa mama zetu. Ndio kimbilio la lishe salama kwa mama zetu. Tukubaliane, tusaidiane, tuunge mkono jitihada za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanaokataa kodi hii wanataka kuirudisha nyuma Serikali hii, hilo hatutakubali. Hatutakubali kurudi nyuma tunakwenda mbele, mbele kwa mbele. Tumetoka katika matatizo makubwa sana ya kutokuwa na mapato, sasa tunaanza vyanzo vipya, lipa kodi yako ya simu, tumia simu yako unavyopenda ukitumia kidogo utalipa kidogo ukitumia sana utalipa sana wala halina mjadala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mitandao sasa hivi kuna tools za kujua every user kwa kila mtu wa mtandao wa simu. Kwa hiyo, wale ambao mapato yao ni madogo watalipa kidogo, lakini wanachangia Taifa lao kwenye maendeleo ya barabara. Atatoka Kivule, Bombambili, atakuja mjini mapema, atakaa Tabata atakuja mjini mapema sababu barabara ni safi za lami kwa hiyo, tuungane na Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema tena na wale wanaoendelea …

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, mnanipotezea muda sasa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Zungu kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tarimba.

T A A R I F A

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nimpe Taarifa Mheshimiwa Zungu kwamba, kodi hii kwa Tanzania haitakuwa nchi ya kwanza, hata Marekani wanatoza kodi kama hii, hivyo, Watanzania wasipate wasiwasi kwamba, sisi tumejitengenezea kodi ambayo ya kumuumiza, bali inachukua at least 19% ya consumer bills katika nchi ya Marekani hivyo Watanzania… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ongea Kiswahili, hatujaelewa hapo ulipoongea kingereza, ongea Kiswahili.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, sijui tafsiri ya consumer bills. Natoka Kinondoni na sijui.

NAIBU SPIKA: Sasa kama wewe hujui na ndio mnasema Kiswahili kifundishwe Watanzania…

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, consumer bills ni gharama za matumizi ambayo ni karibu asilimia 19 ya wamarekani wanalipa kodi hii. Hivyo, Tanzania haitakuwa nchi ya kwanza kuweza kulipa kodi kama hii, ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Sasa hebu ngoja Taarifa yako tuielewe vizuri, samahani Mheshimiwa Zungu. Kule wanalipa asilimia 19 hapa tutalipa asilimia ngapi?

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, hapana, hizo asilimia 19 ni gharama nzima za matumizi ya wananchi wa Marekani katika utilities. Inaonekana ni asilimia 19 imo katika kodi kama hii.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Zungu, malizia mchango wako.

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, nakubali Taarifa yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambazo sasahivi Mkoa wa Dar es Salaam wanataka kuzitengeneza ni zaidi ya bilioni 700. Na hizi pesa zinataka zilipwe, hizi pesa zinakopwa, hizi pesa zinakuja kwa niaba ya Serikali yetu ambayo inasifika kwa kulipa madeni yake na lazima tuchangie tulipe deni hili ili barabara zetu ziweze kuboreka, ili miundombinu ifurahishe na watu waweze kutembea na waweze kupata huduma bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Narudia kusema wanaoendelea kutukana kwenye mitandao mnalipa kodi mjue hivyo. Ahsante sana. (Makofi)
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza nianze kusema kuwa naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze jitihada za Serikali na za Rais katika kuitakia neema nchi yetu, nimpongeze Waziri na Serikali kwa ujumla. Mimi nitajikita sehemu moja tu, sehemu ya mapato na hasa nitajikita kwenye sehemu ya makampuni ya simu nchini mwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano mdogo tu, ukichukua watu milioni 10 kwa mwezi, katika hawa kila mmoja wao akitia vocha sh. 1500 kwa wiki, natumia kiwango cha chini sana, sh. 1500 kwa wiki, kodi ya Serikali ni sh. 450 kwa watu milioni 10. Kwa wiki hiyo ni bilioni nne na milioni mia tano, kwa wiki nne kwa sh. 6,000 tu ambazo anachangia yeye kwa kupiga simu kwa mwezi, Serikali inakosa bilioni 216. Pesa hizi zinakwenda kwenye Makampuni ya Simu, pesa hizi hazirudi Serikalini kwenye excise duty na VAT ya 30%. Mfano mdogo, ukinunua bundle ya sh. 20,000/= unapewa package ya shilingi 19,000/=, sasa najiuliza VAT na excise duty ya Serikali inakwenda wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, inaelekea pesa za Serikali zinatumika kunufaisha makampuni haya, huku Serikali yenyewe haipati kitu. Udhaifu upo kwa regulator. Regulator anatakiwa aingie katika mitambo ya makampuni haya ajue namna gani kodi ya Serikali inapotea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wanalipa 10,000/= kwa mwezi, 10,000/= kwa mwezi kodi ya Serikali ni shilingi 3000/=, kwa mwaka ni bilioni 360 zinaondoka, hakuna mtu anaye-monitor pesa hizi. Makampuni ya Simu wanapolipa kodi zao hawaweki separation za aina za kodi, corporate tax, VAT, excise duty na kodi zingine zote wanaziweka pamoja wanasema tunalipa bilioni 100, bilioni 50, lakini kuna pesa nyingi za Serikali zinapotea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka majibu, tunataka watu wa TCRA na Waziri wa Fedha yuko hapa, haya tumeyasema miaka yote, mwaka huu tunamwambia mwenyewe Mheshimiwa Rais, udhaifu ambao upo kwenye kukusanya mapato ya Serikali kwenye Makampuni ya Simu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Management fee three percent, matangazo ya makampuni haya ya simu yanapewa mpaka asilimia10 ya mapato yao. Kwa hiyo, kama kampuni inachukua asilimia10 kama kampuni inatangaza mapato yake kwa mwaka mathalani bilioni 100, bilioni 10 inakwenda kwenye matangazo. Matangazo yapi ya kwenda nchi hii kwa bilioni 10 kwa kampuni moja? Nataka nipate maelezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la frequency za 4G, nataka Serikali iniambie nchi nyingi duniani 4G ambayo ni long term evolution, baada ya hii 4G sasa hivi itachukua miaka mingi sana kuleta mtandao huu wa 4G. Wenzetu wanapiga mnada, wanampa mtu mmoja, yeye ndiye anawapa wengine, anapewa mnada, Waingereza wanauza 4G mpaka milioni 300 pound, 600 billion. Nchi ya jirani hapa walijaribu jaribu wakapata bilioni 110, nataka kujua TCRA masafa haya wanampa nani na wanapata nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mtambo wa Call Accounting System, tunataka kuwa na forensic audit ya mtambo huu tujue unafanya kazi vipi. Haiwezekani wenye Makampuni ya Simu wanakuwa na ujanja zaidi ya mtambo huu na katika lugha ya kitaalam wanasema garbage in, garbage out, anaye-feed mtambo huu tunataka atueleze anafuatilia vipi mapato ya Makampuni haya ya Simu. Nchi yetu ina uwezo wa kukusanya mapato makubwa sana kwenye Makampuni ya Simu kama regulator TCRA atafanya kazi yake ipasavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kudhibiti mapato ya Serikali na hasa nazungumzia VAT na excise duty, lazima sasa TCRA waweke utaratibu. Makampuni haya ya Simu sasa waweke software system ndani ya mashine zao, ili wakati mtu ana- top up simu yake, ukiweka 10,000 kwenye simu yako, pale pale mashine ya simu yako ifanye kazi kama EFD ioneshe asilimia 30 ya Serikali. Hii ndiyo njia peke yake ya kudhibiti wizi unaofanywa sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiweka sh. 10,000 na simu ikakuambia sh. 3,000 ya Serikali, sh. 7000 yako na operator kila mtu atajiona ufahari namna gani anachangia pato Serikalini. Hili kama halikufanywa tunamwambia tena Mheshimiwa Rais, hili ni jipu. Tunapoteza mapato mengi sana, TRA wanashindwa kudhibiti pato hili, TCRA wenyewe wanashindwa kudhibiti pato hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri wa Fedha yuko hapa tena huyu Waziri wa fedha tulikuwa naye kwenye Kamati ya Kodi, haya yote tuliyasema wakati akiwa mshauri wa uchumi, Ofisi ya Rais, sasa umeingia hapa Mzee, fanya hii kazi naomba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitoa wazo hapa kwenye Bunge Januari mwaka huu kuhusu sekta isiyo rasmi. Sekta isiyo rasmi nchi ya jirani inakusanya kodi pato la Serikali trilioni nane, daladala hizi, bodaboda hizi, wafanyabiashara wadogo wadogo wote hawa walelewe, najua haitawezekana kwa mwaka mmoja, jibu lililotolewa hapa na wataalam ni bughudha kwenda kukusanya hela hizi, ni bughudha kwenda kukusanya trilioni nane? Wakati nchi inahitaji mapato?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Watendaji wa Serikali wana tabia ya kuwa na uvivu kwenye kukusanya hizi pesa. Naomba Waziri wa fedha yuko hapa na Waziri wa Mawasiliano, Naibu nafikiri yuko hapa, tujaribu na tufanye tu-embark na process hii ya ku-collect revenue kwa kiwango kikubwa ili nchi hii isiingizwe mkenge kama ilivyoingizwa sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mitambo hii ya kuweza kuthibiti mambo haya ipo TCRA wanajua ipo, tatizo linakuja ni willingness ya kutaka kufanya shughuli kama hii. Kwa hiyo, mimi sina mchango mkubwa sana, nimezungumzia 4G, nimezungumzia mapato, nimezungumzia na kipato cha display ya 30% ya Serikali ioneshwe kwenye simu zetu ili tujue mchango ambao Serikali inapata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itawafanya TRA wala wasipate tabu, wanakwenda tu kwenye system ya EFD wanajua kila siku tunapata shilingi ngapi kwenye 30%. Udhibiti wa credit card tuelezwe, udhibiti wa hizi credit card uko vipi, consignment ikiingia inatolewa bandarini au airport kama mzigo au inatolewa kama value ya airtime inaingizwa nchini, TRA inatakiwa sasa ijue kama consignment imeingia bilioni tano, asilimia 30 ya bilioni tano tayari ni fedha ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natumai leo nasema suala hili nafikiri labda ni mara ya saba au nane toka niingie kwenye Ubunge, sijaona mabadiliko yoyote. Natumaini sasa leo pamoja na Serikali hii na Rais wetu huyu, haya mambo sasa yafanywe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nachukua nafasi hii kukushukuru kwa kuniweka kwenye orodha ya leo ya kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naunga mkono kwa asilimia mia moja hoja ya Waziri. Nachukua nafasi hii vile vile kupongeza jitihada zinazoendelea kufanywa na Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli katika kupambana na kuhakikisha nchi yetu inakuwa kwenye mstari sahihi. Desperate times desperate measures. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ni ndogo tu, ni namna Wizara ya Biashara inaweza ika-sensitize, ikashirikiana na mikoa yote, ni namna gani ya kuweza kusaidia na kunyanyua informal sector katika nchi yetu. Sekta ambayo siyo rasmi kama mama lishe, bodaboda, machinga, welders na vinyozi. Informal sector kwenye nchi jirani hapa, hawa bodaboda, machinga, matatu, welders, mama lishe, vinyozi huchangia dola bilioni nne kwenye pato la Serikali. Pesa hizi kufanya shughuli zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitakupa mfano kwa Mkoa wa Dar es Salaam tuna wafanyabiashara wa informal sector sio chini ya milioni mbili. Fanya kila mmoja analipa shilingi mia tatu tu kama ada ya ushuru kwa siku mamlaka zinazohusika zitapata milioni mia sita kwa siku, kwa mwezi ni shilingi bilioni 18, kwa mwaka shilingi bilioni 216. Kama kuna programu ya kuhakikisha wanawekwa katika mazingira mazuri tunapata shilingi bilioni 432 kwa kipindi cha miaka miwili tu kwenye informal sector kwenye Mkoa wa Dar es Salaam. Pesa hizi zinakuwa ringfenced, zinalindwa, wanaanzishiwa majengo mapya ya kisasa na kufanya biashara katika mazingira mazuri. Pesa hizi zinaweza zikatumika kuanzisha benki ya wafanyabiashara wadogo wadogo, pesa hizi zinaweza kutumika wafanyabiashara hawa hawa wadogo ambao ndiyo shareholders wakaji-involve kwenye masuala ya biashara ya kilimo. Ethiopia wameweka programu ya kuwafanya vijana kupenda kilimo. Wamechukua vijana 10,000 miaka minne iliyopita, wamewaonesha kilimo cha kisasa na sasa hivi wanafanya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta isiyokuwa rasmi ikiwezeshwa nchini mwetu, ni dhahabu na ni goldmine katika mikoa yote ya Tanzania. Nataka kujua kuna networking gani inayofanywa katika Wizara ya Nishati, Wizara ya Kilimo na Wizara ya Biashara? Wizara hizi tatu lazima ziwe pamoja kama alivyosema Mheshimiwa Serukamba lazima, tuwe na raw materials na vitu vyote vitapatikana kwa networking ya Wizara hizi tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Serikali ijaribu kutazama sekta isiyo rasmi ambayo tunaiona ni bugudha, tunaiona ni sekta ya kufukuzana nao mitaani, tunaiona kama ni sekta ambayo ni parasite wakati sekta hii ikisimamiwa vizuri inaweza ikatoa mchango mkubwa sana kwenye Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, zao la alizeti mwaka huu nchi nzima kila mkoa uliolima alizeti wamepata bumper harvest lakini wanakatishwa tamaa na mafuta yanayoagizwa nchi za nje. Naomba Serikali ijaribu kudhibiti tunyanyue watu wetu, tuzuie product kutoka nje na tuweze kuwasaidia katika agro-industries. Soko la mafuta ya chakula linapatikana DRC, Rwanda, Burundi na katika region yote hii ya East Africa na ni soko kubwa sana ambalo litawanyanyua hawa wakulima. Kwa hiyo, naiomba Serikali na Waziri wa Biashara yuko hapa ajaribu kutazama masuala haya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali mjaribu kutazama namna gani mtanyanyua informal sector. Mjaribu kutazama namna gani one stop center ya kuleta wawekezaji nchini mwetu itarahisisha uwekezaji kwa kuangalia policies na sheria ambazo zitawavutia.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno haya machache, mimi sina mengi, mara nyingi nachangia kidogo kuwaachia nafasi watu wengine, nashukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. MUSSA A. ZUNGU - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MAMBO YA NJE, ULINZI NA USALAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kukushukuru lakini niwashukuru Wabunge wote na Mawaziri wa Kamati yetu ambao wamefanya kazi ambayo ilikuwa mimi ndiyo niifanye. Niwashukuru kwa majibu mazuri, sahihi na wamechukua muda mzuri kunipunguzia kazi yangu mimi hapa leo kwa mujibu wa kanuni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumza machache tu na la kwanza ni la kesi kuchelewa mambo ambayo hayakuzungumzwa humu ndani. Hivi karibuni Waheshimiwa wote mmeona kuwa Mheshimiwa Rais amechagua Majaji wapya wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa ili ku- speed up kesi za watuhumiwa mbalimbali. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hatua yake hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tulishauri kwenye Kamati Waziri aanze sasa kutumia Mobile Court ambayo leo imezinduliwa rasmi na Mheshimiwa Rais. Mahakama hii itasaidia kwa haraka sana kupunguza msongamano wa mahabusu wenye kesi zile ndogo ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kwa vile Waziri wa Mambo ya Nje hakuwepo ni suala nililozungumza sana kuhusu gharama za kodi za nyumba ambazo Serikali inagharamia sasa hivi. Nimezungumza kwenye speech yangu kwa takribani miaka kumi sasa tunatumia zaidi ya shilingi bilioni 216 kulipia kodi za mapango. Serikali sasa iingie kwenye utaratibu wa mortgage financing, utarabu ambao utapunguza gharama kubwa sana ya ujenzi kwani badala ya pesa kwenda huko zitafanya kazi nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mdogo ni jengo letu la Msumbiji. Sasa hivi tuna ghorofa tisa pale Msumbiji, tuna majengo New York na maeneo mengine ambayo ni mali ya Serikali ya Tanzania. Maeneo haya sasa yamesababisha hata maduhuli kuwa mengi kutokana na kodi ambayo tunaikusanya katika majengo hayo na katika nchi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo machache, niwashukuru Mawaziri, Waheshimiwa Wabunge na wewe pamoja na Sekretarieti ambayo imesaidia Kamati yetu kutekeleza kazi kwa mujibu wa sheria zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako sasa lipokee taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na likubali maoni na mapendekezo yote ya Kamati kama yalivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kukushukuru sana. Kwanza naunga mkono asilimia mia moja hoja hii ya Waziri wa Ulinzi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Wananchi wa Tanzania lina history kubwa sana duniani siyo Tanzania tu. Jeshi hili limefanya kazi kukomboa nchi nyingi sana chini ya Jangwa la Sahara. Jeshi hili la Tanzania limefanya kazi kwa uadilifu na kwa ujasiri mkubwa sana kukomboa na kufanya kazi Afrika. Mimi nampongeza sana Mkuu wa Majeshi na Makamanda wake wote kwa namna walivyotuweka na namna walivyoweka nchi hii kuipa heshima. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Jeshi hili ni jeshi kubwa sana mpaka Umoja wa Mataifa wanalitumia kwenda kulinda amani nchi zingine. Jeshi hili ni imara na linafanya kazi kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba kumkumbusha Mheshimwa Waziri, mimi nilikuwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ulinzi, Usalama na Mambo ya Nje kwa miaka kumi toka mwaka 2005 mpaka 2010. Tumejenga hoja na tumekubaliwa na tukaambiwa na tuliishauri Serikali pensheni za vyombo vya ulinzi zitolewe kwenye utumishi wa kawaida, Serikali walikuwa tayari wameshaandaa Muswada kuja Bungeni, lakini walikuwa wanasubiri kidogo wenzao wa upande wa pili na wao waweke inputs zao. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninamuomba Mheshimiwa Waziri kipindi sasa kimefika, siyo jambo zuri kuona vikosi hivi au wanajeshi wetu, maafisa na wapiganaji kutokupata pensheni nzuri sababu tu ya mfumo wa utumishi uraiani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nitakuomba utueleze leo mmefikia wapi kuhusu kulifanya sasa Jeshi la Ulinzi na vyombo vya ulinzi kwa ujumla, viweze kupewa pensheni maalum kwa heshima na kazi kubwa wanayoifanya kwa Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, najua Serikali ina nia njema na tunaamini ina ina nia njema, tunaomba sasa nia njema ile iwekwe ili iweze kuwasaidia wanajeshi hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nchi nyingine kwa mfano Asia, majeshi yanapewa miradi maalum yaweze kujiendesha na kusaidia mapato wanayopata kwenye miradi ile waweze kusaidia kujiendesha kwa namna ambayo wanaona inawafaa. Kuna nchi ya Asia, majeshi yamekabidhiwa kwa kwetu hapa tunaita National Housing, sijui kwa kwao wanaitaje, karibuni nyumba nyingi za mjini nchi zingine zimeachiwa jeshi kuziendesha ili na wao waweze kunufaika.
Mheshimiwa Spika, najua kuna miradi siku za nyuma walipewa Jeshi, najua kulitokea matatizo lakini siyo sababu ya kuwanyima kuwapa fursa hiyo wao kuendesha miradi ili waweze kupata heshima na waweze kujipatia kipato cha kuendesha mambo yao.
Mheshimiwa Spika, nchi zote duniani Jeshi linashirikishwa kwenye masuala ya Contagious Disease Centre (CDC) lazima jeshi liwepo. Sasa sidhani kama kwetu wanashirikishwa. Jeshi wanatakiwa washirikishwe kwenye tafiti mbalimbali za kilimo, afya na za magonjwa; ndiyo wao wenye utaalamu wa kuweza kuchambua na kuisaidia Serikali kufanya tafiti bora, Jeshi letu lina uwezo mkubwa sana wa kufanya mambo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tuliomba kwenye Kamati yetu ya Ulinzi siku za nyuma kuwa Jeshi sasa lipewe jukumu la kufanya doria na kulinda ridge ambazo zipo baharini zinazotafuta tafiti za gesi. Ma-ridge hayo ya ajiri makampuni kutoka nje, wanatumia silaha nyingi sana katika maji yetu na sidhani na kama ipo control, fine, lakini tunazungumzia pato ambazo Jeshi letu lingeweza kupata kwa kufanya doria kwenye ridge hizi ambazo zipo kwenye maji ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Jeshi lina uwezo wa kupata mapato makubwa sana badala ya pesa hizi kutumiwa na makampuni ya nje kama Black Water na makampuni mengine ambayo yanakuja kulinda na yanalipwa pesa nyingi sana. Insurance hii inalipwa na Serikali ya Tanzania kwenye gharama za kutafuta gesi hii. Ni bora sasa na naamini kwa vifaa ambavyo tunavyo, Jeshi sasa lina qualify kwa asilimia mia moja kulinda bahari zetu, kulinda na mitambo hii ya ridge ya tafiti za gesi ili kuongeza usalama lakini vilevile kupata mapato ili na wao waweze kujiendesha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilikuomba muda mfupi tu kwa sababu mara nyingi sichangii maneno mengi huwa nachangia point tu ambazo ni muhimu. Nitamuomba Mheshimiwa Waziri atupatie majibu haya.
Mheshimiwa Spika, lakini niendelee kusema Bunge hili tuendelee ku-support Jeshi, Bunge hili tuendelee kusaidia maslahi ya wanajeshi. Bunge hili lisaidie Jeshi letu liendelee kung‟ara Afrika na Mataifa ya nje. Lidumu Jeshi letu, idumu Tanzania.
Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza nichukue nafasi hii kuunga mkono hoja za Kamati zote tatu. Pili, niwapongeze Mawaziri wa Wizara zote tatu kwa kazi nzuri wanazofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza tena Waziri wa Michezo, takribani miezi minne nilitoa hoja kuhusu Uwanja wa Taifa kutokuwa na sehemu ya kivuli kama mvua zitanyesha. Immediately kazi inafaywa na nafikiri mechi ya tarehe 16 watu tunaokaa katika maeneo yale hata ikija mvua tutakuwa tunasheherekea ushindi wa timu yoyote itakayojaliwa na Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, FIFA ina standard ya viwanja ndiyo maana inaleta fedha kutengeneza viwanja katika miradi ya FIFA. Vipo viwanja vinachezewa Premium League vina hali mbaya sana, vinaharibu ubora na viwango. Mfano jana, kwa dhati kabisa nasema, Uwanja wa Singida ambapo jana Club za Yanga na Singida United wamecheza hauna sifa wa kuchezewa mashindano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimwa Waziri, najua TFF ni watu independent lakini ninyi ndiyo custodian na ndiyo mnasimamia viwango vya Watanzania. Timu ambazo zipo kwenye Premium League na viwanja vyao ni vibaya wahamishiwe viwanja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni jambo la kusikitisha sana jana kuona klabu kubwa kama Dar Young Africans inashindwa kucheza kandanda yake. Naomba wanaohusika walione hili kwa sababu kwenye mpira kuna formation, kuna diagonal attack, diagonal defence, kama kiwanja kibaya, maana kama kule Mbondole kuna kiwanja ambapo kipa wa huku hamuoni kipa wa kule, wanaulizana vipi huko? (Kicheko/Makofi)

MBUNGE FULANI: Ngapi huko?

T A A R I F A

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nafikiri Mheshimiwa Waziri amenielewa.

MBUNGE FULANI: Taarifa umeipokea?

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Kwa Morogoro nimeipokea. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu unajikita kwenye masuala ya viwanja ambavyo havina ubora, Serikali iingilie kati iambie TFF viwango vya wachezaji vinakufa…

T A A R I F A

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, hata usinihoji, sipokei taarifa yake. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, viwanja hivi ndiyo vinatoa ubora wa wachezaji wa Timu ya Taifa, viwanja vibovu vyote pamoja na cha Singida na viwanja vingine vya timu zinazoshiriki Premium League kama Mkwakwani Tanga, vilabu vile vihamishiwe kwenye viwanja vingine ili ubora na viwango vya mpira viweze kupatikana Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na pia namshukuru Mwenyezi Mungu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naunga mkono bajeti hii ya Wizara ya TAMISEMI kwa asilimia mia moja. Nina hakika kwa Mawaziri hawa na usimamizi mzuri utakaofanywa wataweza kufanikiwa kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nachukua nafasi hii kupongeza Serikali kwa kuweza kuingia mkataba na Serikali ya China kujenga reli ya kati nchini mwetu. Hili jambo sio la mchezo. Kwanza tumeweka pesa zetu, wadau wa nje wakashawishika na wao kuleta pesa zao kwa asilimia zaidi ya mia moja. Napongeza sana jitihada zilizofanywa na Mheshimiwa Magufuli pamoja na Serikali yote na Waziri Mkuu kwa namna reli hii itakavyojengwa. Reli hii ita-capture biashara katika nchi nyingi sana ambazo zinatuzunguka. Uwezo wa reli hii kubeba mizigo ni zaidi ya tani milioni kumi kwa mwaka. Reli hii katika kipindi cha miaka saba mpaka kumi gharama zote za deni zitalipwa. Kwa hiyo, naomba tuendeleze amani, amani za majirani zetu ndiyo amani yetu sisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto za elimu bure ambapo ni kazi yetu kuzifanyia kazi ili tuzimalize. Suala la madawati si suala la Serikali peke yake, ni suala letu sisi wote, wa vyama vyote vilivyoko nchini mwetu. Tushirikiane na Serikali yetu tutafute njia mbadala. Watoto hawa ni wetu, mtoto wa mwenzio ni wako. Kwa hiyo, suala la elimu bure na hii changamoto ya madawati tuisaidie Serikali, tuje na hoja positive za kuisaidia Serikali iweze kutatua tatizo hili na changamoto hii iishe ili watoto hawa waweze kusoma na nchi yetu iweze kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sina mchango mkubwa kama kawaida yangu, nazungumzia Benki ya Wananchi ya Dar es Salaam (Dar es Salaam Community Bank). Benki hii imeanzishwa kwa mtaji wa Halmashauri nne, Halmashauri za Manispaa ya Ilala, Kinondoni, Temeke na Jiji la Dar es Salaam. Tume-sacrifice miradi yetu kuweka mtaji kuanzisha benki hii. Hawa watendaji wa sasa hivi walikuwa wanakuja pale Jiji mikono nyuma wanaomba kazi. Baada ya Halmashauri hizi nne kujinyima kwenye vyanzo vyake, tumewanyima wananchi wetu mikopo kwa kutegemea benki hii sasa iwe chombo cha kusaidia wakazi wetu kuwakopesha ili na wao wanyanyue maisha yao. Asilimia kubwa ya mtaji wa benki hii imefanywa na wananchi wa Dar es Salaam wenyewe kupitia kwenye Halmashauri zao. Ni wanyonge ndiyo waliochangia benki hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini habari ya benki hii baada ya wataalam hawa kuingia, baada ya ya benki kusimama kwa hela za wananchi wa Dar es Salaam wenyewe ikiwa kama ndiyo mchango wa kwanza, wameanza kutuingiza katika masuala ya financial regulations, kuna masuala ya mitaji na kipindi kile walisaidiwa wakaanza kutu-dilute. Mtaji wetu sasa hivi wa Halmashauri hizi nne umeshuka mpaka sasa ni asilimia tisa. Wametutoa kwenye umiliki wa benki hii mpaka kutufanya sasa ni watu wa chini kabisa wa benki hii. Benki hii ilifanya mambo haya kwa kutumia vigezo vya mitaji ambayo Halmashauri na uwezo mdogo wa watu kuelewa masuala ya financial services na banking zilivyo hawakuelewa na kila mwezi kila kwenye mikutano mikuu tukanza kushushwa mpaka sasa hivi hatuna mali, hatuna chochote kwenye benki hii. (Makofi)
Naiomba Serikali Mheshimiwa Waziri na wewe ni mtaalamu wa majipu, tunataka benki hii ifanyiwe uchunguzi, tunataka benki hii iende kwa CAG ili sasa hatma na heshima ya wananchi na Halmashauri hizi nne za Dar es Salaam zirudi kumiliki benki hii kama tulivyoianzisha. Haiwezekani wenye mtaji, watu maskini wanyang’anywe benki hii, ni dhambi kubwa sana ambayo imefanywa. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri ulichukue hili, kwa vile benki hii imechangiwa na Halmashauri zako, naomba sasa lifanyie kazi ili tuweze kuimiliki benki hii na kuichukua tena iwe mali ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya machache, naunga mkono hoja. Kama kawaida yangu mimi huwa nasema kidogo lakini nasema makubwa. Nakushukuru na nina-save muda ili wengine nao waweze kuchangia.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri na Naibu Waziri wake kwa kazi nzuri wanazofanya, kwa kweli Waziri na Naibu wapo karibu sana na Wizara hii na wadau wote wa michezo na sanaa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, Rais juzi alimzawadia Peter Tino shilingi milioni tano na hali ya wachezaji wetu wa zamani ambao wamecheza mpira miaka ya 1980 ni mbaya sana. Mheshimiwa Rais ameonesha njia, najua TFF inajitawala haiko chini ya Wizara, lakini Wizara ndio custodian wa michezo nchini.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Wizara, wawashauri TFF katika bajeti zao angalau wachezaji walioshiriki timu ya Taifa miaka ya 1980 ambao sidhani kama wamebaki hata 10 au 15, najua yupo Manara, Kitwana na Mbwana nafiriki bado yupo, wawapatie bima kuwasaidia wachezaji hawa kwa mateso wanayoyapata sasa hivi mitaani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona Jellah Mtagwa namna alivyotumikia Taifa katika michezo hasa mchezo wa mpira. Katika miaka ya 1990 na 1980 Jellah Mtagwa alitumika picha yake kwenye stempu za Tanzania; Shirika hili la Posta sasa hivi lina wajibu wa kumkumbuka Jellah na kumsaidia kwa mateso ya magonjwa ambayo anayo sasa hivi. Ushauri wangu TFF iwakatie bima wachezaji wote wa zamani ambao wako hai ili waepukane na mateso ya maradhi ambayo wanayapata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile wachezaji wote waliocheza timu ya Taifa upo wajibu wa TFF kuweka majina yao kwenye uwanja mpya wa Taifa ili kuwa-inspire wachezaji wapya na wakumbukwe kwa picha na majina kwa namna walivyochangia ushindi. Wapo wachezaji waliocheza goal stage bado wapo ili na wao waonekane na vijana wetu wawe inspired na wachezaji wetu wa zamani.

Mheshimiwa Spika, lingine ni Bodi ya Ligi ya TFF; tumeona namna wanavyo-approve viwanja vibovu vichezewe ligi. Wachezaji wakicheza kwenye viwanja vibovu na ambavyo vingi vipo wanaumia sana. vilabu hivi vinapata gharama kubwa sana kutibu wachezaji ambao wanacheza na wanaumia kwenye viwanja vibovu vya premium league. Naomba bodi hii sasa ivifungie viwanja vyote kwa msimu ujao ili kila kiwanja kiboreshwe na kitengenezwe vizuri na wale ambao viwanja vyao havitafungiwa watafute viwanja mbadala kuepuka wachezaji kuumia na viwango vyao kunini.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii tena kumshukuru Rais kwa namna alivyochangia AFCON U-17 alitoa bilioni moja, tumefungwa, lakini tusikate tamaa bado tunayo nafasi. Vijana hawa wapewe moyo; hamasa zilikuwa nyingi, lakini maandalizi yetu hayakuwa mazuri. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kumshukuru Waziri na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na nataka kuwaambia wenzangu Wabunge na wananchi tuipe muda Serikali, hii ni bajeti ya kwanza na ni bajeti mpya baada ya kutoka kwenye uchaguzi. Tumetumia gharama kubwa sana kuleta demokrasia nchini mwetu, tumetumia pesa nyingi sana mwaka wa jana, tuipe muda Serikali, the best is yet to come, nawaahidi mambo yatakuwa mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuunga mkono hoja naiomba Serikali i-revisit upya suala la kukata kodi kwenye kiinua mgongo cha Wabunge. Nia njema ya Serikali ambayo ipo, lakini Serikali naiomba i-revisit. Kwa wastani Wabunge tunalipa kodi kwa miaka mitano tuko Bungeni hapa takribani milioni 50, inafika, I stand to be corrected kama utaweza kunirekebisha, lakini kwenye hesabu zangu tunalipa almost milioni 50 kwa miaka mitano ambayo tunakaa hapa Bungeni. Kwa hiyo, naomba Serikali wajaribu kuitazama hiyo upya.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni la kuongeza kodi kwenye mitumba. Hili ni agizo la Afrika Mashariki, ziko nchi kwenye Afrika Mashariki zina viwanda vya nguo, sisi hatuna, hii ni ajira ya vijana wengi nchini mwetu. Hawa vijana wakihangaika na biashara zao wataweza ku-create disposable economy. Wakipata chochote na wao watanunua soda, watanua cement, watachangia kodi kwenye kipato ambacho watakipata kwenye kuuza nguo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali wai-revisit hii kodi mpya kwa kutazama namna gani ajira zitaathirika katika nchi yetu. Yako malalamiko wananchi wanasema sisi Wabunge tunasema kodi hii ya simu, mimi nasema ni sahihi iwepo na ndiyo njia peke yake ya Serikali ya kupata mapato ya ziada. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, transaction ya M-PESA nchini mwetu kwa mwaka ni trilioni 50, trilioni 50 transaction ya pesa zinazozunguka kwa mwananchi na mwananchi mwenzio ni fifty trilioni kwa mwaka. Makampuni haya yana-lobby kuona kuwa wanaoumia ni maskini, si kweli watakaoumia ni wao. Kwa hiyo, kodi hii naiunga mkono, Serikali iendelee na kodi zingine na kukamata mapato kwenye simu, we are losing a lot of revenue kwenye maeneo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye simu kuna non voice revenue, haya ndiyo maeneo Serikali inatakiwa ikae iyatazame. Pesa nyingi sana zinapatika kwenye non voice revenue ambayo sheria zetu hai-capture, inafanya makampuni haya yanaondoka na hela nyingi. Mfano mdogo, Kenya walilalamikia wananchi, lakini Kenya they put their foot down kodi ile ye transfer imewekwa na leo M-PESA, Safari com peke yao wameongeza wateja 21 percent kama hii inaumiza wananchi Kenya wangesema.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wetu na sisi tubadilishe minding setting zetu, Waheshimiwa Wabunge tusiwe na tabia ya kizamani ya kuona tukilipa kodi watu wanaumia, bila kodi Serikali hii haichapishi note. Simu hizi unakaa Dar es Salaam unapeleka pesa Jimboni within second hivi kulipa hata shilingi 400, 500 kwa kila transaction tatizo liko wapi? Ukienda Ulaya Dollar to Pound shilingi ngapi tunakatwa, ukienda Ulaya Dollar to Euro shilingi ngapi tunakatwa, commission za bureau de change, kwa nini tunaogopa kulipa kodi za Serikali? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Kenya, Safari com peke yake imepata faida ya six hundred billions kampuni moja, sisi Makampuni yetu miaka yote yanapata hasara. Kwa hiyo, Serikali put your foot down, kamata hizi kodi ili wananchi wapate huduma. Pia regulator TCRA lazima wajue teknolojia inavyobadilika business as usually imekwisha, wawe on their toes kuhakikisha makampuni haya yanalipa hizi kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja kwenye extractive industry transparency initiative kwenye madini. Nchi yetu ni ya tatu katika ku-export gold lakini utajiri huu haurudi kwa watu, haurudi kwa watu kutokana na baadhi ya policy zetu ambazo haziumi. Leo Tanzania katika nchi 182 ni wa 152 katika human development index, this is wrong. Haiwezekani nchi yenye madini kama haya tuwe 152 katika nchi 185 katika human development index.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka 2010 Tanzania ime-export trilioni tatu na bilioni mia tatu ya dhahabu, pato la Serikali mpaka 2010 was only seven percent, bilioni 220. Hii inatokana na matatizo ya multinational corporate, misinvoicing, ku-abuse transfer pricing. Kama Serikali tunazo policy nzuri lakini tunakuwa tuna-mismanage eneo hili sababu ya under staff na capacity ya watu wetu kuweza kujua hivi vitu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2002 mpaka 2011 tumepoteza trilioni 18, eighteen trillion kwa misinvoicing, makampuni haya wajanja sana wa kuleta mitambo mikubwa kudanganya bei ambazo watu wetu hawana capacity ya kujua. Kwa hiyo, naiomba Serikali badala ya kuingia kwenye VAT za tourism, kamateni hela huku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, abusing ya transfer pricing bado ipo, share zinauzwa, mamlaka zinazohusika hazifuatilii, lingine adhabu kali tunazo, zitumike.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna conversion on mutual administrative assist in tax kama Serikali imesahau Waziri wa Fedha ataniambia hebu ai-note hii kitu na Mwanasheria Mkuu yuko hapa. Conversion on mutual administrative kwenye kodi, hiki chombo hatuja ki-sign, kama tumeki-sign na kwa vile hatukukisaini hatupati information ya makampuni haya ya disclosure za kodi zao kwenye nchi zao. So we are losing money simply sababu hatuja-sign huu mkataba, tuki-sign huu mkataba tutasaidiwa kuambiwa kampuni fulani ina- disclose nini kwenye nchi zao.
Kwa sababu nchi zao wameweka sheria lazima u-disclose activity unaifanya kwenye foreign country ili na wao waweze kubana kulipa kodi, kama imefanywa fine kama haijafanywa kwa nini haijafanywa? Inawezekana haikufanywa au imechelewesha kufanywa kwa sababu mambo haya tunafahamu ya mishemishe ambayo kila mtu anayajua, lakini with this Government kama haijafanywa ifanywe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni shida kubwa sana, lakini niipongeze Serikali kwa kuwa na mpango wa Sovereign Wealth Fund kwenye gas and oil. Wenzetu Trinidad na Angola wamefanikiwa kwenye rating za confidence za investors. Wameweza kuweka five billion kwenye accout zao za mfuko wa baadae wa vizazi vyao kwenye Sovereignty Fund za nchi zao, inaleta confidence, inapunguza inflation ya pesa zetu ambazo tunazipoteza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, TMAA, auditors wa Madini wanafanya kazi nzuri sana nchini lakini TRA wanatakiwa wawe zero distance na hawa watu ili wanapotoa ushauri waende wakakamate kodi kwenye extractive industry.
Nakushukuru naunga mkono kwa asilimia mia moja.
Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nami nachukua nafasi hii kukushukuru, lakini vilevile lazima kwanza tukubali. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna alivyouona na namna alivyoshaurika. Namshukuru Mheshimiwa Mkapa, Mheshimiwa Msigwa kasema tusikatae kwa sababu tu kuna watu wamesema tuukatae. Tunaukataa kwa sababu mkataba huu ni non starter kwa Tanzania.
Mheshimiwa Spika, if you don‟t deal with the problem, the problem will deal with you. Hili ni tatizo kubwa sana. Sasa kuna mjumbe amesema tunaukataa kwa sababu kuna watu, viongozi wetu wamesema. Ni kweli viongozi wamesema na wamesema sahihi. Sasa hapa kuna kiongozi kwenye Bunge EU kuna kamati mbili; International Trade na International Development. Hizi kamati nazo hazielewani kuhusu mkataba huu. International Trade wanaushikilia mkataba huu na International Development hawautaki mkataba huu.
Mheshimiwa Spika, sasa kuna mtu kasema tunawasikiliza watu, tumsikilize Mbunge wa European Union anachokisema kuhusu mkataba huu. Anasema: “the agreement to pose a risk to regional economies as their infant industries will face unfair competition due to products from the European Union.
Mheshimiwa Spika, huyu ni Mbunge wa European Union, siyo Mtanzania wala hatoki East Africa. Anasema, she point it out that the European Union had pushed a hard bargain in the deal large by arm twisting Kenya.” Wamewafuata Kenya wakawapinda mkono. Anaendelea kusema, “I think this kind of agreement is unfair for the East African Region; Europe is pushing very hard stance and they have taken Kenya as a leader. Kenya is the only one that has interest in this trade agreement, because they are not a list development country.” Kenya ni non list development country. Siyo list kama sisi.
Mheshimiwa Spika, anasema, Kenya need this agreement to maintain acces to the European Union. Anaendelea kusema; “if the agreement goes through, you East Africans;” anatuambia sisi, hawaambii Kenya, anatuambia wote block, “have no more preferences; you will receive all products coming from Europe in your market which will promote unfair competition.
Mheshimiwa Spika, European competence is high, ni kweli! Hivi maziwa ya salsa yatakuja hapa, wanakuta maziwa yametoka Ulaya ya dola moja badala ya haya ya kwetu ya dola moja na nusu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili jambo wenyewe wanatutahadharisha. Wanaendelea kusema, so far they have been able to guarantee Kenya access to the EU market without even this agreement.
Mheshimiwa Spika, umeona tunapopelekwa? Kenya kusaini huu mkataba au wasiusaini, tayari wana soko EU. Kwa hiyo, they don‟t need this agreement. We have guarantee Kenya! Hao ni EU wanasema, that we still have access to the European market and to help their market in internal African Market.
Mheshimiwa Spika, mengi tutayasema, nchi hii tukiingia kwenye mkataba huu, tumeua industries ambazo sasa hivi Serikali inataka kujenga.
Mheshimiwa Spika, wewe ni mmoja wa watu ambao wameijengea heshima kubwa sana nchi hii. Kwenye mikutano ya EUSP - Brussels, ndio ulikuwa unasimama na kutuongoza sisi kupinga kitu hiki cha kutuingiza katika matatizo makubwa sana. It goes without saying. Tukisaini mkataba huu, we are done.
Mheshimiwa Spika, illegal fishing inayofanywa kwenye bahari zetu. Tuna-lose 250 million Euros kwa kila mwaka kwa samaki kupelekwa Soko la Ulaya. Samaki hawa wanaibiwa katika bahari zetu, samaki hawa wakifika kwenye Soko la Ulaya wanatozwa kodi kule; na kodi hiyo inabadiki kutumika kwa wananchi wa European Union, sisi hatupati chochote. Nilitegemea kwanza angesema wange-deal na samaki zinazoibiwa kwetu kabla hazijapelekwa kwao kutumia kwa watu wao.
Mheshimiwa Spika, mkataba huu unasema, kukiwa na loses za revenue wataweka mfuko. Hebu tujiulize Waheshimiwa Wabunge, zipo nchi zimeshasaini mkataba huu; Caribbean countries; Mauritius hapa Afrika na kuna nchi za Afrika Magharibi zimeshaanza ku-lose revenues.
Mheshimiwa Spika, masuala ya industries katika nchi zao zimeshaanza kupotea. Mfuko huo walisema unaanzishwa, haujaanzishwa, haupo kwenye bajeti na hakuna popote katika nchi hizi zinazosaidiwa. Sisi wa tatusaidia lini?
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mkataba ni mzuri sana, kwa lugha nzuri iliyoandikwa kisheria, lakini it is a non starter kwa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba Waheshimiwa Wabunge, nchi hii tusimame pamoja kwenye suala hili; one Nation under one God, tusikubali kusaini mkataba huu. Kama kuna nchi imesaini, wana interest zao.
Mheshimiwa Spika, kuna nchi nyingine hawana interest za Kitaifa, wana interest zao binafsi. Tunajua nchi zilizoingia kwenye mikataba hii wanafanya biashara individually, lakini tuulize, soko la maua pesa ngapi zinarudi Kenya na pesa ngapi zinabaki huko zinapopelekwa? Hatutaki kuingia kwenye matatizo kama ya Kenya.
Mheshimiwa Spika, yote haya tunavyosema hapa kwamba Kenya inatumika as a front as a leader ni kuhusu malighafi ambayo Tanzania inayo, nothing else. Na wewe uliwaambia Brussels mkitaka madini yetu, jengeni viwanda kwetu. Tatizo liko wapi? Badala ya kusafirisha madini kutoka hapa kuyapeleka Ulaya, walete viwanda hapa, tuta-promote jobs, tutaweza kupata revenues za kutosha na kusaidia nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, sina haja ya kusema mengi, hili suala linafahamika, na yule anayepinga hili, analipinga tu kuonesha kwamba anasimama, anapinga. Hawana hoja ya msingi.
Mheshimiwa Spika, naunga mjono hoja, tusisaini mkataba huu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, na momi nachukua nafasi hii kukushukuru kunipa nafasi, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kwanza nitoe pongezi za dhati kwa Serikali, Mheshimia Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mheshimiwa Waziri mwenye Wizara hii kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Lazima tuwapongeze sababu Wizara hii imeshika mambo mengi kwenye nchi lakini bado inafanya kazi vizuri sana, lazima tuwape pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mabadiliko makubwa sana yamepatikana kwa kipindi kifupi sana toka Mheshimiwa Rais aingie madarakani na hasa alivyompa Wizara hizi tatu Mheshimiwa Mbarawa. The Country is progressing sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajikita kwenye maeneo yale ya siku zote, yapo mabadiliko kidogo tumeyaona, lakini Mheshimiwa Waziri nilitaka nikwambie sijui kama ulishawahi kuona kiti kinawahi kukamata mshahara wa Waziri; na Kiti kikikamata mshahara wa Waziri ujue kura ikipigwa ujue Kiti kitasema nini. Haya mambo tunayasema; kuna mtu juzi nimekutana naye anasema wanashukuru Ethiopia imewafungua macho kwenye mambo ya simu. Tumeyasema haya miaka mitano hamjafungua macho? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi na kuomba Mheshimiwa Waziri ni mchapakazi vizuri sana, cash cow ya Tanzania sasa hivi ni Shirika la Simu la TTCL. Kama tumeweza kununua ndege zetu, ni hatua nzuri sana ambayo Serikali imeifanya, ni lazima tui-bail out TTCL ili nayo iweze kutoa mchango mkubwa sana wa GDP kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi wana utawala mpya, kuna CEO mpya kijana, kabobea, taaluma zake anafanya kazi vizuri, Chairman mpya kachaguliwa mzuri, wanachohitaji ni affirmative action ya Serikali katika kuwasaidia. Sasa mimi nakuomba Mheshimiwa Waziri tupate majibu mazuri kuhakikisha TTCL kweli inasaidiwa na Waheshimiwa Wabunge tuwe mabalozi wa TTCL ili tuweze kusaidia Serikali yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, TTCL ni shirika la umma, its high time Serikali ikaipa exclusive rights za TTCL ku-handle masuala yote ya IT Nchi nzima badala ya kutegemea wakandarasi binafsi. Leo Serikali ina-share asilimia 39 mpaka 40 Airtel. Toka Serikali iweke pesa zake Airtel hakuna faida yoyote ambayo imekuwa decrared na Kampuni hii. Kwa nini sasa Serikali isitoe pesa zake ikaziingiza TTCL ili Shirika hili liweze kubobea? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitoa ushauri hapa kuhusu TCRA sasa wazibane kampuni za simu kwenye correction za kodi za Serikali kwenye VAT na excise-duty ziwe displayed kwenye simu kuonesha kweli kodi ya Serikali inapatikana. Lakini bado napata kigugumizi, hizi display kwenye simu zetu hazina feed kwenda TRA. Kwa hiyo, TRA hawana taarifa ya kodi inayokusanywa, huyu mkandarasi ambaye aliyepewa kazi hii ya TTMS there is something wrong with this thing.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtambo huu ni mali ya Serikali kwa asilimia mia moja, umenunuliwa zaidi ya miaka mitatu/minne iliyopita, leo mkandarasi anauendesha kwa kulipwa four percent kwa mwaka. Mikataba mingi kwenye mtambo huu bado inatia mashaka Serikali kukusanya mapato yake. Sasa Mheshimiwa Waziri ndiyo nakwambia Kiti kikikamata mshahara wako usilalamike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi napata taabu, unapoona mtambo wa TTMS ambao umenunuliwa na Serikali unaendeshwa na mkandarasi for all this time, why? Hivi hatuna local staff? Kwenye mkataba hakukuwa na package ya ku-train Watanzania wakauendesha mtambo huu? Na TCRA wameonyesha udhaifu mkubwa sana wa kuweza kuingia kwenye Network Operating Centre za operators. Na kwa vile hawaingii kwenye NOC za ma-operator hawawezi wakakamata line zote na miamala yote ya simu inayopita kwenye mtambo huu. Hamuoni haya Mheshimiwa Waziri tunasema haya miaka mitano?(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna teknolojia mpya kila siku zinazaliwa, sasa imekuja IOT (Internet On things), nafikiri unaijua. Ni makampuni machache sana wanajua na wanafanya na wame-introduce software hii kwenye soko. Software hii wapewe TTCL ili waweze kushirikiana na maeneo ya kukusanya kodi kama vile TRA, waingie kwenye mitambo kwenye operating centres za makampuni ya simu. Sababu IOT ni mtandao maalum ambao mashine hizi zinazungumza wenyewe kwa wenyewe bila binadamu kuingia ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mashine hii ita- sense kuna transaction inafanyika hapa itabidi itume ile message ipeleke TRA. Kwa hiyo, mimi nakuomba Mheshimiwa Waziri kama mnataka mfano wa Ethiopia ambayo ndio juzi mnaambiwa wamefanikiwa, reli ile imejengwa kwa kusimamiwa na Kampuni ya simu ya Ethiopia. Leo Ethiopia inatengeneza vifaa vya Jeshi vya kisasa vyenye standard ya NATO, pesa zinatoka kampuni ya simu. Hivi tunangoja nini na leo Mheshimiwa Rais amezungumza asubuhi? Hivi kwa nini Serikali Mawaziri msimsaidie Rais ambaye ana uchungu wa mapato nchi hii? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mikataba hii ya simu bado tuna-weakness kubwa sana. Makampuni haya yamepewa ten percent deduction ambayo wana redeem kwenye gross turnover yao kwenye masuala ya matangazo. Hii lazima ipitiwe upya ipunguzwe. Makampuni ya simu haya yamepewa three percent kwenye management fee. Mheshimiwa Waziri wewe unajua mambo ya simu, management fee three percent ya turnover ya kampuni ya simu ni pesa nyingi sana, ndio maana utasikia unaambiwa sasa hivi your call is not reachable, yule mtu anayezungumza anazungumza nchi nyingine. Hela inatoka hapa analipwa mtu inakuwa recorded kwenye eneo lingine, hebu pitieni tena haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imenunua ndege, ndege nzuri, mimi ni mtaalamu wa masuala ya ndege. Ndege hizi zina STOL (Short Take off and Landing) zinaweza zikatua kwenye kiwanja cha mpira. Kwa abiria haiwezekani lakini kwenye dharura kwenye mambo muhimu zinatua na zina-take off kwenye kiwanja cha mpira kwa kuweka flats forty degrees down. Lakini zina advantage vile vile zinabeba abiria wengi, sabini na sita, nautical mile moja kwa gharama ya mafuta kwa kiti inalipa vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, management mpya, bado kuna tatizo la Serikali kuboresha baadhi ya viwanja vya ndege. Ndege hizi zina uwezo wa kuruka twenty four seven Mheshimiwa Waziri. Service ya ndege ni hourly bases, item za ndege zinakwenda kwa masaa, kama ndege hairuki kile kifaa hakitumiki. Sasa kwenye viwanja vyetu vya ndege vingi, unless uniambie mmeshafanya maana Bunge lililopita nililisema hili wakati huo I think Naibu Waziri alikuwa Tizeba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kitu kinaitwa PAPI (Precision Approach Path Indicator) ambayo inamsaidia rubani kutua. Tumenunua ndege za gharama kubwa sana ni lazima tuwe na usalama wa ndege na abiria. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MUSSA . ZUNGU: …Dakika kumi tayari? Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na hatimae niko ndani ya ukumbi huu wa Bunge nikiwa na afya ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono bajeti ya Wizara ya Afya kwa asilimia mia moja. Kwa nini naunga mkono bajeti ya Wizara ya Afya? Nitumie fursa hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu na Baraza lote la Mawaziri bila kuwasahau Mheshimiwa Ummy na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla. Mmefanya kazi kubwa ambayo inaonekana kwa muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mfupi mmeweza kugawa ambulance 67 katika baadhi ya Halmashauri zetu. Kwa muda mfupi mmeweza kutoa vitanda 20 vya kulalia wagonjwa, vitanda vitano vya kujifungulia, magodoro yake na mashuka 50 kwa kila Halmashauri zetu. Kwa hilo, nawapongeza sana na nawatia moyo pigeni kazi tupo pamoja na ninyi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nirudi katika Mkoa wangu wa Shinyanga, niwasemee wanawake wa Mkoa wa Shinyanga walionileta ndani ya ukumbi huu. Najua Wizara ya Afya hamjengi miundombinu katika hospitali zetu, lakini ndugu yangu Mheshimiwa Ummy wewe ni ndugu yangu sana, kwa hili naomba unisamehe. Pamoja na yote unayoyafanya na pamoja na jitihada zote za ambulance, sijui vitanda na nini kama hamtokaa sawa na TAMISEMI hakuna ambacho kitawezekana. Hivyo vitanda vitakuwa havina pahala pa kuviweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hilo kwa sababu gani? Miaka mitano iliyopita kila nikisimama ndani ya bajeti hii huwa nasema ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga na suala hili halijawahi kuchukuliwa hata siku moja. Najua siyo la Wizara ya Afya lakini kwa sababu Mheshimiwa Simbachawene yupo hapa na sikupata nafasi kusema TAMISEMI naomba niliseme. Hamtutendei haki Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, tumeanzisha ujenzi kwa nguvu zetu wenyewe, lakini hakuna fedha ambayo tunapewa kutoka Serikalini. Tukipewa fedha tunapewa fedha kidogo, tutamaliza lini ujenzi wa hospitali hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeanzisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, toka tumeanza kila mwaka tunapewa shilingi bilioni moja, ujenzi huu utakamilika lini? Ndiyo maana ninasema Mheshimiwa Ummy na Mheshimiwa Kigwangalla pamoja na jitihada zote bila kukaa sawasawa na TAMISEMI yote mnayoyafanya hayatakuwa na maana yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba pamoja na kwamba ni Wizara ya Afya nitaomba TAMISEMI watujibu ni kwa nini Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kila mwaka hatupewi pesa kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga inahudumia wagonjwa wengi zaidi kwa sababu Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga na Manispaa ya Shinyanga hatuna Hospitali za Wilaya. Kwa hiyo, inabeba mzigo mkubwa ambao haikustahili kuubeba. Hospitali hii ya Mkoa wa Shinyanga pamoja na kuhudumia wagonjwa wote hao x-ray machine ni mbovu, hazifanyi kazi, kila zikitengenezwa zinaharibika. Kuna kampuni inaitwa Phillips wala hawaonekani kwenda kutengeneza mashine hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapata taabu kidogo, kwa sababu nikienda Hospitali ya Kahama hawana x-ray machine, Hospitali ya Wilaya ya Kishapu hawana x-ray machine na nikienda Mkoani x-ray machine ni mbovu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake hawa na wananchi wote wa Mkoa wa Shinyanga wanakwenda kupata wapi huduma za x-ray? Namuomba Mheshimiwa Waziri wa Afya akija atuambie wanaiangaliaje Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga kwa kuiletea x-ray machine mpya kwa sababu hii ni ya muda mrefu na imekwishachoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Mkoa wa Shinyanga haina vifaa vya upasuaji, ninaiomba Wizara ya Afya, kwa sababu hospitali hii inabeba Mkoa mzima na uzito mnauona, tunaomba Wizara ya Afya mtuletee vifaa vya upasuaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Mkoa wa Shinyanga inaitwa Hospitali ya Rufaa, inapaswa kuwa na Madaktari Bingwa 21, mpaka hivi ninavyoongea ina Madaktari Bingwa watatu tu. Sasa madaktari hawa wanafanya kazi kwa kiasi gani? Ninakuomba sana Waziri utakaposimama utuambie, ni lini mtatuongezea Madaktari Bingwa katika hospitali ya Mkoa wa Shinyanga, kwa sababu hawa waliopo hawatoshelezi hata kidogo. Kinachonisikitisha zaidi katika hawa watatu hakuna hata Daktari Bingwa wa Wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee kuhusu vya vituo vya afya, Mkoa wa Shinyanga tuna vituo vya afya 21, katika vituo hivi ni vituo vitano tu ambavyo vinatoa huduma ya upasuaji. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 76 nimeona amesema kwa mwaka huu wa fedha wataboresha vituo 150 vya afya kwa kuwa na majengo ya upasuaji. Nikupongeze Mheshimiwa Waziri na watendaji wako wote kwa jambo hili kubwa ambalo mnakwenda kulifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kubwa sasa ni lini utekelezaji huu utaanza? Tunaposema tunakwenda kupunguza vifo vya mama na mtoto ni kupeleka huduma ya upasuaji kwenye vituo vyetu vya afya. Bila kuwa na huduma ya upasuaji kwenye vituo vyetu vya afya vifo vya mama na mtoto vitazidi kuongezeka. Ninakuomba Waziri utuambie hivi vituo 150 ambavyo umevisema kwenye hotuba yako ni lini utekelezaji wake utaanza? Niwashukuru sana lakini niwaombe Serikali iangalie kila mwaka ijaribu kuboresha vituo vyetu vya afya tulivyonavyo ili viweze kutoa huduma zinazostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mgawanyo wa watumishi. Nasikitika kusema kwamba mgawanyo wa watumishi hauko sawasawa. Ukienda maeneo ya mijini watumishi unawakuta wako wengi, unakuta labda hospitali inahitaji watumishi labda 30 lakini wapo 50, kwa nini? Hamtutendei haki tunaoishi maeneo ya vijijini. Ninaiomba Wizara na wanaohusika mtuangalie hata tunaotoka maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini watumishi wengi wanakwenda maeneo ya mjini na maeneo ya vijijini tunakosa watumishi. Naomba hili mliangalie kwa makini ili na sisi wananchi wetu waweze kupata huduma zinazostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niongelee kuhusu maendeleo ya jamii. Katika Mkoa wa Shinyanga kuna vituo vya wazee viwili, kituo cha Kolandoto na Usaanda. Bajeti iliyokwisha nakumbuka kuna fedha zilitengwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya wazee ingawa hazikuainishwa zinakwenda kujengwa wapi, naomba Waziri akija aniambie, kile Kituo cha Kolandoto ambacho hali yake ni mbaya sana, majengo karibu yanadondoka, Wizara inafikiria nini kuboresha majengo haya ya wazee ambao kwa kweli yanasikitisha na yanatia huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mtuambie maendeleo ya jamii vituo hivi vya wazee mnafikiria lini na fedha zake zipo wapi kwa ajili ya kuwaweka wazee wetu katika mazingira mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kusema haya yote nirudi kwenye Mfuko wa Wanawake katika Halmashauri zetu. Fedha zinazotoka maendeleo ya jamii kwenda katika Halmashauri zetu sielewi kidogo ni kwa nini usimamizi wake unakuwa mgumu na mbaya. Kuna fedha zinazotoka Wizarani na kuna fedha zinazotoka Halmashauri, ninawaomba Wizara Halmashauri isipotoa fedha zake za asilimia kumi ya mapato ya ndani msiwape fedha za Wizarani. Kwa sababu mnapokuwa mnawapa fedha kutoka Wizarani ndipo wanapokuwa na jeuri ya kutokutoa ile asilimia kumi ya mapato ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja, Waheshimiwa Mawaziri pigeni kazi, Mwenyezi Mungu atawabariki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa sababu muda wangu ni mdogo, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri. Nawapongeza Serikali lakini tupongeze na jitihada za Mheshimiwa Rais kutaka ku- excel uchumi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna ndege nzuri, jana nilikuwa nasikia mtu anasema ndege hizi hazifai. Ndege hizi zina store equipment system ambazo zina-show take off na landing, zinafaa kwenye viwanja vyetu vidogo ambavyo haviwezi kubeba ndege ambazo zinachukua runway ndefu sana. Kwa hiyo, tupongeze jitihada hizi za ndege hizi kuweza kutumika katika viwanja vingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ndege hizi hazitumiki sawasawa kwa sababu viwanja vyetu havina ubora wa kupokea ndege husika. Hata viwanja vingine, kuna kipindi viwanja vyetu vinashindwa kuchukua ndege au ndege kutua kutokana na hali mbaya ya hewa, simply kwa sababu hatuna transponder instrument landing system ambazo katika mazingira ya hali yoyote ya hewa ndege hizi zinaweza kutua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze ku-capitalize matumizi ya ndege hizi, kitaalam ndege huwa haipumziki, kinachopumzika ni rubani na crew ambao wako kwenye ndege. Kwa hiyo, tungekuwa na viwanja ambavyo vina taa, instrument landing system, precision approach path indicators na vertical approach slope indicators, itasaidia ndege hizi kuwa capitalized na kutumika kwa kipindi chote 24/7. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri alizingatie hili aboreshe viwanja ndege ziweze kuruka kwa usalama wa abiria, vifaa vyenyewe na viwanja vya ndege vyenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la reli hii ya SGR, ni hatua kubwa sana ambayo tumepiga na naipongeza Serikali. Reli hii kama haina mizigo itakuwa haiwezi kufanya kazi vizuri, haitaweza kulipa deni kwa muda unaotakiwa. Solution ya reli hii ni mizigo na bandari ya Dar es Salaam iko congested.

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya kuwa kuna utaratibu wa mazungumzo lakini yasiwe taratibu. Mpaka leo ujenzi wa bandari ya Bagamoyo bado hakieleweki, bila bandari hii reli yetu itakosa mizigo na tutashindwa kurudisha pesa hizi mapema, tusiogope kukopa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali ijaribu na wataalam ambao wapo na wazuri wakae na mwekezaji wakubaliane twenty equivalent units za makontena yatakayoingia kwenye bandari ni mangapi, waweze kujua wharfage ya mwekezaji ni ngapi na duty ya Serikali ni ngapi. Tukienda hivi tutafanikiwa kujenga reli na bandari kubwa ya kisasa ya kuweza kubeba mizigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imekumbwa na mafuriko, mafuriko hayana nguvu mbele ya utaalam na engineering ya binadamu. Katika Bonde la Msimbazi ambalo linaanza kutoka Segerea linakwenda Surrender Bridge. Jambo ni dogo sana, Serikali wametuambia katika mpango wa DMDP wana mpango wa kuboresha mto huu, lakini wanakopa hizi pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako watu ambao wamejitokeza ambao watalipa fidia na kutengeneza miundombinu ya mfereji huu, kwa nini hawa watu wasipewe kazi hii? Kwa nini Serikali mkope halafu katika kukopa kwenu hakuna component ya fidia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wananchi hawa hawatalipwa fidia sisi hatutakubali. Tunataka wananchi wetu walipwe fidia kwa sababu they have been there for the last sixty years. Kama kuna mtu kajitokeza ni bora afanye yeye na Serikali mkope kwa kufanya mambo mengine ili wananchi hawa waende katika sehemu bora zaidi na kuendeleza maisha yao. Hawa ndiyo watu walionipigia kura mimi lazima niwatete. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Dodoma - Dar es Salaam imeshakwisha, iko congested na ni ndogo. Namwomba Waziri, tayari wako watu wamejitokeza wa Kuwait Fund kui-finance barabara hii, wazungumze nao ili waweze kujenga barabara hii kwa njia sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno hayo, nikushukuru sana na naunga mkono hoja kwa kazi nzuri anayofanya Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa dakika hizo.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajielekeza kwenye masuala ya infrastructure na hasa Bagamoyo kama ulivyosema wewe na baadhi ya Wabunge.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwako, sasa hivi lazima tuwe na new thinking kwenye economic corridor nchini Tanzania. Bila kuweka new thinking tutaendelea kuwa waoga wa kufanya maamuzi, kutoa ushauri na kuirudisha nyumba hii. Uzalendo haimaanishi kukataa kila kitu, lazima tuwe na calculated risk. Risks hizi zinapimwa na zinaweza zika-work Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwako; negotiating team hii ya Tanzania ipate fursa ya kuja kwenye Bunge lako, ikae na Wabunge wajaribu ku-brainstorm na kusaidia nchi yetu iweze kwenda mbele na hasa kwenye mradi huu wa Bagamoyo. Infrastructure za nchi nyingi sana zimeendeshwa na gold backed currency; deposit ya gold na baadhi ya madini nchini mwetu yanaweza kutumika ku-fund infrastructure katika nchi yetu. Naomba wataalam wa nchi yetu watazame suala la gold backed currency ili kuweza kujenga taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napongeza watendaji wa Serikali, nampongeza Waziri, naipongeza Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya. Mchango wangu ulikuwa ni huo tu, Bunge lipate nafasi kukaa na team inayo-negotiate Bandari ya Bagamoyo ili tupeane taarifa mbalimbali na tu-move this country forward. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ukilelewa kwenye vyombo hivi toka udogo wako, unajua nchi ilivyokuwa imara na ilivyokuwa salama. Mimi nilijiunga na Jeshi la Anga wakati nina miaka 18 tu na katika umri wangu mpaka nakuwa mtu mzima nilikuwa katika vyombo hivi. Kwa hiyo, najua umuhimu wa vyombo hivi na ulinzi ambao nchi hii sasa hivi unao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna alivyoweka kipaumbele masuala ya ulinzi wa nchi yetu. Siyo kila kitu Kamati inaweza kuleta kwenye Bunge kuzungumza mambo ya ulinzi, lakini niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, nchi iko salama na kuna mambo makubwa yanafanywa na Serikali kwenye vyombo hivi katika mambo ya kiusalama ambavyo vinafanya Taifa letu kuogopwa katika nchi ambazo zimezunguka. Demarcation za nchi zetu zinalindwa na vyombo hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jeshi letu lina uwezo wa rapid deployment forces, any time any place nchini mwetu, lakini nidhamu ndani ya Jeshi ni kubwa sana. Nampongeza CDF, Chief of Staff na Makamanda wote wa JKT na Makamanda wengine kwa namna wanavyoweza kuhimili na kusimamia ulinzi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jeshi sasa lina utaratibu wa vifaa kama mavazi, kushonwa nchini Tanzania. Tutaokoa pesa nyingi sana za kigeni badala ya kuagiza uniform ambazo zimeshashonwa nje ya nchi. Napongeza sana utaratibu ambao umewekwa na Serikali, Mheshimiwa Rais, Waziri na Jeshi lenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fidia ya Naval Base Kilwa ni kipaumbele kikubwa sana cha Kamati na Mheshimiwa Waziri wa Fedha yuko ndani hapa. Mahsusi kwenye Kamati ya Bajeti nimejenga hoja hii, pesa zinazohitajika ni shilingi bilioni 3.6 tu. Tuchukue kituo hiki licha ya kuwa ni cha ulinzi kitakuwa na uwezo kuwa na commercial activities.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama kubwa sana za dry dock, za seaworthiness ambazo meli nyingi zinahitaji Tanzania, zinakwenda kutengezwa nje ya nchi. Tumezungumza na Naval Commander watakuwa na uwezo wa kuweka dry dock katika eneo hili iwe kitega uchumi kikubwa sana cha vyombo hivi vya ulinzi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha, aone kuwa anawekeza katika sehemu ambayo watakuwa na own source na uwezo wa kuwa na mahitaji yao kwa siku za mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni tamaduni za nchi nyingi; ukienda Pakistan, wana kitega uchumi, kama sisi hapa tunayo hii National Housing Corporation. Ukienda Pakistan, National Housing Corporation ya kwao iko chini ya vyombo vya ulinzi ili waweze kujihimili na mahitaji muhimu. Umeona hapa Majenerali waliostaafu malipo yao yanachelewa. Kwa hiyo, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri wa Fedha aone umuhimu wa kuweza kulipa hizi pesa ili kituo hiki kiweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilibahatika kuwa katika Kamati hii toka Bunge la Tisa, la Kumi na sasa la Kumi na Moja. Kuna issue ya Sera ya Ulinzi, bado inaelekea upande mmoja wa Muungano hawajairidhia na kuipitisha. Tunaomba Serikali zishirikiane, pande zote mbili hizi wakae, wamalize ili sasa National Defence Act iweze kupitishwa na iwe dira ya kuweza kusaidia maslahi na mambo mbalimbali ya ulinzi katika nchi yetu. Mheshimiwa Waziri wa Nchi yuko hapa, ajaribu kuzungumza na upande wa pili waweze kumaliza haraka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya Jeshi kwa mwaka huu ni shilingi trilioni tatu, lakini ceiling waliyopewa iko chini ya hiyo shilingi trilioni tatu. Tunaomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha aone umuhimu. Jeshi wakati wa amani linakuwa ni jeshi la uchumi. Chombo hiki, ni jeshi mashine. Kwa hiyo, naomba, najua amenipa dakika tano na sina nia ya kuzungumza mambo mengi sana, nisije nikasema mazuri ya ulinzi ambayo nayajua halafu yakaharibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waziri wa Fedha ashirikiane na chombo hiki kusaidia Jeshi hili liweze kufanikisha mahitaji yake kipesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya machache, naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya SADC ya Usimamizi wa Mazingira kwa ajili ya Maendeleo Endelevu (The Southern African Development Community SADC – Protocol on Environmental Management for Sustainable Development)
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kabla ya yote kwanza nichukue nafasi hii kupongeza Serikali kwa kuleta maazimio haya yote, na naunga mkono maazimio yote haya matatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia Azimio la Montreal; kuna mashirika ya ndege sio chini ya 25 mpaka 30 yanatumia anga la Tanzania, na kila abiria anatakiwa alipe kodi ya carbon emission (carbon emission tax). Nataka kuuliza Serikali, wamejipanga vipi katika kudai pesa hizi ziweze kurudi nchini na kuboresha mazingira ya Mlima Kilimanjaro, tukapanda miti zaidi ya bilioni moja, kwa sababu ndege hizi zinaharibu mazingira yetu hapa nchini. Kwa hiyo, naomba Serikali walione hilo; kama tunalipa kodi na ndege zinatumia anga zetu ni bora tukatafuta namna ya kudai pesa hizi ili zirudi hapa nchini mwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kuhusu depreciation ya ozone; depreciation ya ozone inatokana na mambo mengi, pamoja na friji. Nchi nyingi zilizoendelea sasa hivi wamepiga marufuku kutumia friji aina ya Freon; hizi friji zimepigwa marufuku nchini mwao lakini zinaletwa nchini mwetu, na zikija kwetu zinaharibu mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuelimisha wananchi wetu waelewe; hivi sindano ambayo imetumika Ulaya utakubalije Tanzania itumike kama sindano mtumba? Na sasa hivi magari mengi yataacha kutumia petroli na fossil fuels, wataanza kutumia umeme na gesi, magari haya yana hatari ya kuja katika Bara la Afrika na kuharibu mazingira yetu. Kwa hiyo, naomba kama wenzetu Ulaya wamekubali sasa kutumia HFC 134a, tetphoroicine, na sisi tukubali kuacha kutumia freon gas kulinda mazingira ya Taifa letu na Bara la Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nikushukuru kwa kunipa nafasi, nimshukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na wataalam wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa maslahi ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze mwongozo wa Mheshimiwa Rais kwa kuongoza nchi iwe na mwelekeo wa viwanda, iwe na mwelekeo wa kizalendo kwa watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina-introduce Electronic Tax Stamp (ETS) ni jambo ambalo zuri sana na ukitizama tumechelewa, lakini uhakika wa source ya revenue ya Serikali utapatikana kwa utaratibu wa mfumo huu wa Electronic Tax System (ETS). Lakini nilitaka kujiridhisha tu au Serikali imejiridhisha vipi na huyu aliyepewa kazi hii, due diligence ilifanywa na nani? Kwenye semina tumeambiwa wamefanya Mabalozi, lakini ukitizama taarifa mbalimbali, hii kampuni ina matatizo makubwa. Hii kampuni ina kesi Morocco, wamefanya price offering mara kumi zaidi ya nchi zingine walizofanya kazi hii. Kampuni hii inachunguzwa na Bunge la Kenya, kwa malpractice. Kampuni hii imeziangusha Serikali zingine kutokana na mfumo wake wa malpractice na corruption. Sasa Mabalozi hawa waliofanya due diligence ya kampuni hii, mimi nitapenda waitwe waje waulizwe taarifa zao walizipata wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulifanya semina; TRA na Wabunge na hoja zilizoulizwa na Wabunge kwenye semina Serikali walizi-defer, walishindwa kuzijibu. Kutokana na hoja za msingi za kizalendo ambazo Wabunge wameuliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, TTCL chombo cha umma, kwa gharama za mradi huu wa bilioni 48, mimi binafsi naomba Serikali i-revisit mpango wake wa kuajiri watu wa nje kusimamia makusanyo ya kodi nchini Tanzania. Unapo- surrender sovereign ya tax regime ya nchi kwa kampuni ambayo tayari ina matatizo makubwa kama haya duniani na sever ya kampuni hii ni mali ya vendor mwenyewe. Naiomba Serikali tena na nia njema ku-support mpango huu wa ETS, lakini bado ningeomba shughuli hii ifanywe na TTCL ambacho kina uwezo, chombo cha umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unaposema information za vendor huyu zitakwenda kwenye data center, kuna njia nyingi sana za ku-under declare traffic kwenda kwenye data center ya Serikali. Kuna command nyingi sana za mitandao unaweza uka-hide information zingine. Kwa hiyo, mpango huu ni mzuri naunga mkono asilimia 100, lakini naomba Serikali i-revisit jambo la ku-surrender regime ya tax kwa Kampuni ya nje ambayo tayari ina misuguano kwenye nchi nyingi sana. Kwa hiyo, naomba kazihii nzuri, ni muhimu kwa Taifa letu lakini wapewe TTCL.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2008 tulishauri Serikali kuhusu masuala ya wizi wa declaration za traffic kwenye mitandao ya simu. Serikali ikanunua mtambo, walituambia walinunua mwaka 2008 kumbe hawakununua, walimuweka Mwekezaji ambaye kaja na mtambo wake wa gharama za 50 billion wakaingia mkataba wa miaka 15, which was very wrong. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, masuala ya mitandao server kama ni mali ya vendor utapigwa tu na tumepigwa na tunaendelea kupigwa. Kwa hiyo, hoja yangu tulihoji hata gharama ya mtambo wenyewe na huu mkataba kwenye semina tumeambiwa ni miaka mitano. Miaka mitano mtu anasimamia sovereign ya regime ya kodi nchini na hakuna popote ambapo tumepewa comfort ya forensic audit ya mtambo wake atafanya nani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna nchi nyingi wameweka hii system, kuna kitu kinaitwa new generation quickly response, hoja kubwa ni makusanyo lakini ku-cub na kuzuia elicit goods katika soko ambalo ni jambo zuri sana. Mitambo hii inayowekwa sasa hivi huu sijui, kwa new generation mimi na wewe ukienda dukani unatumia app yako ya simu kuweza kuona stamp ile na goods ambazo ziko mitaani ni genuine. Sababu stamp za mitaani ambazo siyo genuine hazitakosa ku-have return ili kuthibitisha unatumia simu yako una-log kwenye ile code ya stamp inakwambia hii ni genuine au siyo genuine. Sasa tulitaka kujiuliza mtambo huu ambao Serikali wanatuambia walishainigia mkataba unayo app kama hii ambayo kujiridhisha mfanyabiashara, consumer kuweza kujua hii stamp iliyowekwa hapa ni kweli stamp ya Serikali na mwananchi wa kawaida anaisaidia Serikali kwa kwenda katika maduka au katika supermarket aki-log in pale pale na simu yake na yeye anapewa majibu kuwa hii ni stamp ya Serikali au ni stamp ya mitaani, nilitaka kujua hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, server inapokuwa ni mali ya vendor si rahisi kwa TRA au Serikali kujua under declaration ya ripoti yoyote ya vendor, siyo rahisi. Kwa hiyo, nilikuwa naomba, naunga mkono mpango huu naunga sana 100 percent. Ombi langu uwekezaji huu ni mdogo sana,
tuiwezeshe TTCL ifanye hii kazi siyo chombo kutoka nje.
(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bombardier mpya zinatolewa Q400 New Generations, abiria 96 (96 passengers) flies Dar es Salaam - Dodoma siku zote watu wanakosa nafasi. Huduma nzuri, performance nzuri, tukipata Bombardier Q400 New Generations ya abiria 96 gharama za uendeshaji zitashuka, tutakuwa na abiria wengi kwenye ndege. Kwa hiyo naomba Waziri wa Fedha hili nalo alitizime, kuweza kununua New Generation Bombardier Q400 ili tuweze kupunguza gharama za uendeshaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Taarifa ya Kamati ukurasa wa 47 chombo hiki kiendeshwe na mamlaka ya umma ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa dakika tano ulizonipa. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya na maendeleo ya nchi yetu yanavyokwenda chini ya Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka nimshauri, ni miaka mingi tu namshauri Mheshimiwa Waziri kuhusu biashara ya bandari na maeneo mengine ambayo si friendly kwa importers na exporters. Ukichukua mfano wa container la futi 20 ambalo sasa hivi gharama yake kwa Bandari ya Mombasa ni dola 80, wamepunguza kutoka dola 103. Kwa Tanzania container la futi 20 handling charges zake ni dola 170. Sasa hii haiwezi ku-attract importes kutumia Bandari ya Dar es Salaam na kuweza ku-encourage volume ya importation. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bandari ya Dar es Salaam transit goods ambazo ndizo tunazozitegemea, ndiyo uzima kabisa wa bandari yetu, importation container futi 20 ni dola 100 handling charges lakini ukienda Kenya ni dola 60. Kwa hiyo, watu wengi lazima watahamia katika bandari ambayo ina unafuu. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri aendelee kuchukua ushauri wa kutazama ni namna gani tariffs za kodi za importation za bandari zetu zitashuka, ziwe friendly kwa wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine naotaka nimpe Mheshimiwa Waziri ni kutazama gharama za kodi Tanzania. Tulijaribu kumshauri Waziri siku za nyuma ajaribu kutazama na huu ulikuwa ni mpango wa siku nyingi, VAT ilipoanza ilikuwa ni 20%, ikashuka to 18% ilikuwa ni utaratibu wa Serikali kuendelea kuishusha VAT kuja 16% au hata 17% ili ku-encourage industries. Industries zikiwa encouraged ajira na growth zitaongezeka. Kwa hiyo, namuomba Waziri atazame sasa hivi suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, excise duty; soft drinks sasa hivi Tanzania production imeshuka sana kwa sababu gharama ni kubwa na wananchi hawawezi kumudu kununua maji au soda. Excise duty ukiipunguza volume ya mauzo itakuwa na production itakuwa kubwa kwa maana Serikali haitapoteza kitu, itapata mapato yake kwenye consumption tax. Mnywaji akinywa soda au maji kodi inalipwa. Kwa hiyo, naomba Waziri alitazame suala hili ili kuona namna ya ku-encourage growth. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine atazame gharama za importation ya industrial sugar. Wafanyabiashara wengi wanalalamika, wanalipa deposit ya pesa, lakini sasa ni zaidi ya miaka mitatu, minne hawarudishiwi pesa zao na imekwenda juu sasa imefika zaidi ya shilingi bilioni 45 na hii ni mitaji ya wafanyabiashara. Wafanyabiashara wanalipa kodi vizuri, Serikali ikitazama maeneo mazuri ya kukaa na kushirikiana nao mapato mengi ya kodi Serikali itayapata bila kuwa na viwango vikubwa ambavyo vinawakimbiza. Wafanyabiashara wengi sasa hivi wanaondoka kwenda nchi zingine. Ni lazima tu-attract investors kwa kuwa na tariffs nzuri na friendly za kodi nchini mwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Job Yustino Ndugai kwa Uamuzi wake wa Kulifanya Bunge Kutekeleza kwa Vitendo Dhana na Bunge Mtandao (e-Parliament)
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nachukua nafasi hii kukushuru, lakini vilevile kumpongeza Mheshimiwa Spika, kwa uthubutu aliouleta ndani ya Bunge hili na Taifa letu kwa kukubali sasa Bunge liwe Bunge Mtandao kwa jina lingine e-Parliament. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika dunia kuna tathmini zilizofanywa na audit ya World Bank, Tanzania ni nchi ya tano kwa kasi ya kukata miti; na hii ni hatari sana kwa nchi yetu. Miti inayokatwa Tanzania sasa hivi ni kiwango cha kilometa za mraba 15,000 na kwa hatua hii ya Mheshimiwa Spika na hatua ya Serikali na wao vilevile kuingia katika Mtandao e- Government, tutapunguza athari ya mazingira kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru mtoaji taarifa, ametupa taarifa kwamba, sasa hivi Serikali itaokoa zaidi ya shilingi bilioni 100 kwa mwaka katika nyaraka mbalimbali zinazotumika na Serikali kuja Bungeni. Hii ni hatua kubwa sana ya kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Spika, naomba vilevile kutoa wazo kwa Bunge hili na mamlaka zinazohusika, kwa kutumia fursa hii ya e-Parliament tunaweza sasa vile vile tukapata fursa ya kutumia maswali kwa online questions za Wabunge wakajibiwa online na Wabunge wakaweza kutumia maswali haya kupeleka kwa wapigakura wao kwenye Majimbo, kwenye ma-group ili nao wakajua kazi anayofanya Mbunge Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kila mtu anapata fursa ya kuuliza maswali ndani ya Bunge. Kwa hatua hii na kwa siku za mbele, lazima Bunge litakuwa live katika masuala ya mitandao na wananchi watajua wawakilishi wao ndani ya Bunge wanafanya nini na kutekeleza majukumu yao ya Kibunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii tena kumpongeza Mheshimiwa Spika kwa kazi nzuri aliyoifanya. Hongera Mheshimiwa Spika, hongera Serikali, hongereni Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa SADC na kuendesha vyema Mkutano wa 39 wa Jumuiya hiyo
MHE. MUSSA A. ZUNGU – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MAMBO YA NJE, ULINZI NA USALAMA: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kukushukuru tena na kuwashukuru Wabunge Sita waliochangia ambao ni Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha, Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mheshimiwa Amina N. Makilagi, Mheshimiwa Victor K. Mwambalaswa, Mheshimiwa Peter Serukamba, tumemalizia na Mheshimiwa Agness Marwa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha ameunga mkono na ametoa history ya namna Frontline States ilivyoanzishwa, ni kweli zilikuwa ni nchi Tano ni kama vile alivyozisema Tanzania, Botswana, Angola, Msumbuji na Zambia. Ameunga mkono na ameendelea kusema kuwa nchi hizi sasa zikumbuke namna Tanzania ilivyojitoa na tuendeleze kujitoa kuhakikisha sasa tunajitoa kwenye masuala ya uchumi. Mheshimiwa Makilagi nae ameunga mkono, amezungumzia namna Mheshimiwa Rais alivyozungumza kwenye hotuba yake tujitegemee. Mheshimiwa Victor Mwambalaswa ameendelea kutoa history kabisa ya namna Mwalimu alivyopambana na kuzungumza utawala wa kibeberu Afrika uondoke.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ally Saleh naye amepongeza, amezungumza kuhusu namna ushiriki wa Tanzania kwenye Mabunge haya. Hata hivyo, nataka nimkumbushe Mheshimiwa Ally Saleh Wabunge wetu wanashiriki kwenye mikutano ya Bunge la Afrika na hata Makamu wa Rais wa Bunge hilo la Afrika anatoka Tanzania, kwa hiyo hii inaonesha Wabunge wetu wanakwenda na wanashiriki.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Peter Serukamba ameunga mkono, amezungumzia masuala ya uchumi, amepongeza na suala la utulivu wa nchini mwetu, amesisitiza kwa suala la sekta binafsi nayo itiwe mkazo na amezungumzia, amekumbusha kuwa legacy ya Mheshimiwa Rais katika SADC katika mambo yote lakini haitasahahulika kwa Kiswahili kimeweza kuwa kitatumika na kitaweza kukua.

Mheshimiwa Spika, watu lazima wakumbuke Tanzania tunapotoka. Kama mtakumbuka tarehe 11 Novemba, 1965 Rhodesia chini ya Ian Smith walitangaza UDI (Unilateral Declaration of Independence), Tanzania ilikuwa ni nchi ya kwanza kupinga utawala huu dhalimu na Tanzania wakaomba Uingereza wasiitambue Serikali ya Ian Smith ya Rhodesia, lakini Harold Wilson wakati ule akiwa ni Waziri Mkuu wa Uingereza walikataa na palepale Mwalimu Nyerere akavunja uhusiano na Uingereza. Kuonesha namna gani gani Rais Nyerere alikuwa na uchungu na ukombozi wa Afrika, tulikataa misaada kutoka Uingereza. Hii inaonesha namna Tanzania ilivyokuwa mstari wa mbele katika kupambana na udhalimu wa nchi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania ilichelewesha maendeleo yake ili kuhakikisha nchi za Afrika zipate uhuru wake, kwa hiyo damu ilimwagika na watu wengi walipoteza maisha yao. Sasa tunaliagiza kwenye Azimio letu na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kufuatilia hasa maelekezo ya Mheshimiwa Rais kuhakikisha trading within block ya SADC inafanywa na tuna-trade kwa kiwango kikubwa sana.

Mheshimiwa Spika, takwimu zinaonesha sasa hivi ndani ya Afrika tuna-trade kwa asilimia 16 tu, tofauti na nchi za Ulaya zina-trade kwa asilimia 70 wenyewe kwa wenyewe. Ili tujikomboe lazima tuanze kutafuta masoko ya ndani ya kujikomboa na kuhakikisha bidhaa zetu za kilimo na bidhaa zetu nyingine zinanunuliwa na Waafrika wenyewe.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kukushukuru, na sasa niwaombe Wabunge wote kwa pamoja kwa Kambi zote ambazo ziko ndani tuunge mkono azimio hili na tumpongeze Rais wetu kuchukua nafasi ya kijiti hiki na inawezekana akaendelea tena kuchukua kijiti hiki kwa mwaka mwingine unaokuja kutokana na kazi nzuri anayoifanya na kutokana na nchi za Afrika kumkubali na kumtegemea yeye kutuongoza wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utendaji uliotukuka kwa kipindi cha miaka minne ya Uongozi wake
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kuunga mkono hoja muhimu sana ambayo imeletwa leo kwa Rais wetu mpendwa wa nchi hii. Kwa jina safi la Mheshimiwa Rais anaweza kuitwa a man of all seasons, ni mtu ambaye kwa kweli ametuvusha katika maeneo mbali sana.

Mheshimiwa Spika, mapato ya nchi yetu kwa mwaka 2015 tulikuwa tunakusanya bilioni 800, mpaka jana tunakusanya trilioni 1.9, haijawahi kutokea. Hili si jambo dogo ni jambo kubwa. Tunafanya miradi mikubwa sana ya nchi hii, ukichukua Dar es Salaam tuna mradi wa bilioni 600 infrastructure peke yake Dar es Salaam; tuna Salander Bridge; tuna Tanzanite Bridge; tuna barabara za lami kutoka Mbezi mpaka Kibaha, barabara nane. Sasa haya mambo tatizo mabaharia hawaoni haya mambo. Wakiacha ubaharia watayaona haya mambo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nidhamu ya ukusanyaji pesa, nidhamu ya utumishi, nidhamu ya matumizi, sasa hivi Tanzania inang’aa katika nyanja za kimataifa. Bandari yetu imeongeza mapato, bandari yetu imeongeza meli, sasa hivi ukipita maeneo ya Salender Bridge kuna meli kibao zinangoja kushusha mizigo ya nchini na nje ya nchi, nani kama Magufuli? (Makofi)

WABUNGE WENGINE: Hakunaaaa!

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amepita Jela amekuta watu wameonewa ametoa agizo watu wote walioonewa walitiwa ndani waachiwe, nani kama Magufuli? (Makofi)

WABUNGE WENGINE: Hakunaaa!

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amewafuata mafisadi walioiba pesa amewaambia waliokubali makosa warudishe, warudi kwa wake zao. Nani kama Magufuli? (Makofi)

WABUNGE WENGINE: Hakunaaa!

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, Hospitali zimeboreshwa leo Hospitali za Dar es Salaam ukiingia utafikiri uko Ulaya, Hospitali safi, huduma nzuri na madawa kibao yanapatikana.

Mheshimiwa Spika, tuna ndege, kasema hapa juzi Mheshimiwa Waziri, ndege za mizigo. Tuna ndege ambazo karibuni zitaanza kubeba abiria kutoka Ulaya kuja Tanzania kwa utalii, dogo hilo?

WABUNGE WENGINE: Kubwaaaa!

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Magufuli oyeee. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kukushukuru lakini kuzipongeza Kamati zote tatu kwa kazi nzuri waliyoifanya kuwasilisha hapa Bungeni na naziunga mkono taarifa za Kamati zote tatu kwa namna walivyowasilisha na kufanya kazi na kutoa taarifa ya mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAMISEMI ni chombo ambacho kinasimamia asilimia kubwa sana utendaji wa Serikali nampongeza sana Mheshimiwa Jafo na Mawaziri hawa Wawili anaofanya kazi nao pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli ni Wizara ambayo ndiyo ni engine ya Taifa hili, yako masuala ya Elimu, Afya na masuala mengi na hasa mazingira hata sherehe yetu ya mazingira asilimia kubwa ya kazi zetu zinafanywa na Watendaji wa halmashauri ambao wako chini ya Mheshimiwa Jafo na Wizara yake ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawapongeza sana lakini nichukue nafasi hii vilevile kuunga mkono kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kubuni vitambulisho vya Wajasiriamali sasa hivi suala la Wamachinga, Mama lishe katika Mkoa wa Dar es Salaam na Mikoa yote Tanzania usumbufu hakuna tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wakati anafunga Kampeni yake pale Dar es Salaam mwaka 2015 alisema atahakikisha anapiga marufuku mgambo na kweli mgambo wote wamepigwa marufuku na hakuna mgambo yoyote anayesumbua wafanyabiashara wadogo wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara wadogo wadogo sasa na mitaji midogo waliyokuwa nayo wanahakikisha kuwa mitaji yao iko salama na mali zao haziibiwi wala hawadhurumiwi tena. Hii yote ni kutokana na vitambulisho hivi ambavyo Mheshimiwa Rais amewapa vijana wake na wao waone ni sehemu ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuwapongeza wote waliofaulu katika shule zetu za Sekondari kwa mara ya kwanza katika Mkoa wa Dar es Salaam sasa hivi baada ya kutoka division zero sasa hivi wanafunzi wameanza kupata division one na hakuna division zero. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii yote ni jitihada ya Mheshimiwa Rais, Wizara ya Tawala na Serikali za Mitaa kuweka Elimu bure na kuboresha Elimu katika shule zetu. Tumejenga mabweni shule ya Jangwani sababu wanafunzi waweze kusoma na walale kwenye mabweni wasirudi majumbani nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jafo Wizara hii unaitendea haki wewe na Manaibu Mawaziri wako Wawili baada ya maneno hayo naunga mkono Kamati zote tatu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii. Lakini nichukue nafasi hii vilevile kumpongeza Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanazofanya, kwa kweli mnaitendea haki Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, muda wangu mi mdogo tu, nazungumzia suala la LNG ambalo mazungumzo yanaonekana yanachukua muda mwingi. Mazungumzo kuchukua muda mwingi yawe productive, yawe na uangalifu wa kutazama maslahi mapana ya nchi. Na ecosystem sasa hivi imekuwa introduced ambayo badala ya kufanya LNG wanafanya FNG (Floating Natural Gas Products).

Mheshimiwa Spika, na huu ni mtambo ambao unafungwa baharini kulekule kwenye meli na meli inabeba mzigo mkubwa sana wa mtambo huu na gharama za kuzalisha na kusafirisha gesi inakuwa ni ndogo. Na results zake ambazo Serikali itazipata na nafasi ya kutengeneza mtambo huu ni miaka miwili tu, tofauti na miaka tisa ambayo LNG inafanya kuleta kwenye shore ya nchi kavu, kwa hiyo watu wanaona labda ni muda mwingi sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaomba Serikali katika mazungumzo yao wa-incorporate na waone umuhimu wa ku-introduce FNG badala ya LNG. Najua FNG ni component moja, haitakuwa kwa mradi wote, lazima LNG iwepo, lakini tunaweza tukaanza na FNG ili Serikali ikaanza kuvuna mapato yake kwa haraka sana kwa gharama za FDI ambayo ni Foreign Drect Investment, bila Serikali kuweka hela zake. Na wana-estimate FNG kuweza kuiletea Serikali kwa kipindi cha miaka mitatu labda two billion US Dollars.

Mheshmiwa Spika, kitu muhimu kwenye mikataba lazima wataalam wetu wawe na uhakika wa outflow meter waweke digital wireless meters ambazo zina sensor na kuona gas inayotoka. Hata wewe ukiwa ofisini hapa unaweza ukaona sensors za outflow meter ya internet of things ambazo zitakuwa zinafanya kazi huko Lindi, wewe utaona kiasi gani cha gesi kinatoka na hakuna nchi wala hakuna mahali popote wawekezaji hawa wataweza kuiibia Serikali.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, naomba katika mazungumzo mjaribu ku-introduce FNG ili tunaze na FNG Serikali ipate mapato. Na katika kuanza mradi huu Serikali ihakikishe inaweka digital wireless meters za kuweza ku-sense gesi itakayokuwa inauzwa nje ili tusiibiwe katika mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, na mimi nichukue nafasi hii kwanza kukushukuru. Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema; nakishukuru Chama changu cha Mapinduzi na wananchi wa Jimbo la Ilala kwa kunirudisha tena kuwa mtumishi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Rais ametoa hotuba kubwa sana. Ameshatoa vision ya nchi, kazi kubwa sasa ya wasaidizi wa Rais pamoja na Bunge ni kuweka road map ya utekelezaji wa mambo aliyoyatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais, katika hotuba yake aliyoitoa kwenye Bunge hili la Kumi na Mbili, ametoa maelekezo ya kupunguza au kufuta kodi za kero katika utalii. Utalii unaleta fedha nyingi sana Tanzania. Sasa hivi kutokana na Covid 19, watalii wengi ambao walikuwa wanakuja Tanzania, mishahara yao na mapato yao kwenye nchi walizotoka, nazo zimeathirika kutokana na kutokuweza kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali, waanze kufanyia kazi kuona ni kodi zipi za kero wanaweza kuzipunguza. Nataka nijue na niiulize Serikali, je, watalii hao wanaokuja nchini mwetu, mamlaka zinazohusika au Wizara zinazohusika wanayo data ya watalii wanaokuja Tanzania kwa maana ya anuani zao, majina yao na nchi zao ili kuweza kuwafuatilia, kuwasalimia kwenye siku za sikukuu au siku zao za kuzaliwa ili kuweka kama undugu wao na Tanzania ili waweze kuwa na hamu ya kurudi?

Mheshimiwa Spika, taarifa zinasema watalii hawarudi Tanzania. Je, tumejua kwa nini watalii hawarudi? Kama kodi ni kubwa, kama kuna kodi za kero na Rais ameshatoa maono yake, basi wataalam wetu wajitahidi kutekeleza.

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais, kafanya mapinduzi makubwa sana kwenye mapato ya mawasiliano nchini mwetu, makubwa sana. Miaka ya nyuma Serikali ilikuwa haiwezi kuingia kwenye network cooperating center za vendors wa simu kwa sababu walikuwa hawana uwezo huo na Serikali ilikuwa haina appetite na makampuni hayo yalikuwa yanafanya self assessment kwenye kulipa kodi.

Mheshimiwa Spika, leo Serikali hii ya Dkt. Magufuli inaweza kujua every revenue user kwa kila mteja wa simu, kwa maana kodi sasa zinaku-cessed kitaalam na Mamlaka za Mapato. Ndiyo maana mapato ya kodi ya simu yamekuwa makubwa. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuliona hili na ninamshukuru kwa kuanzisha Wizara hii nzuri na imepata Waziri mzuri ambaye anachapa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuwa kwenye shamba la mkonge. Miaka 60 mkonge ulikuwa unazalishwa Tanzania tani 130,000; Watanzania walikuwa 6,000,000. Leo tunazalisha mkonge tani 30,000 na Watanzania tuko milioni 60. Lazima Serikali ije na affirmative action ya kunyanyua mkonge, kunyanyua mazao ya mawese ili Taifa liweze kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba vilevile kuwe na programu ya kuwafanya vijana kupenda kilimo. Tuwe na machinga duka na tuwe na machinga kilimo. Kuna siku zitakuja, walimaji sasa hivi wana umri mkubwa sana. Itakuja kuwa na hatari Tanzania itakosa walimaji kwa sababu vijana wengi hawana programu au mapenzi na kilimo. Serikali ije na programu; Ethiopia wamefanya, wamechukua vijana zaidi ya 15,000, wamewaingiza kwenye programu na sasa vijana wengi wanajua umuhimu wa kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
The Fire and Rescue Force (Amendment) Bill, 2021
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Waziri na Serikali vilevile nishukuru Wabunge waliochangia na Wabunge wa Kamati kwa kazi nzuri waliyofanya kwa kweli they deserve kupongezwa kwa namna walivyoweza kushughulikia Muswada huu kwa haraka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisemi mambo mengi kwa sababu mengi yameshasemwa niko sana katika Kanuni, sheria inasema Waziri akishatunga Kanuni zikishakuwa tabled kwenye Bunge within six days lazima ziwe zimeshawasilishwa Bungeni na Kamati Ndogo ya Sheria iweze kuzifanyia kazi. Niombe tu migogoro mingi mitaani katika nchi yetu sasa hivi inatokana na Kanuni kutokuwa rafiki kwa wananchi kwa gharama kubwa sana ambazo wananchi wanatozwa mfano ukaguzi wa vifaa vya fire katika majengo ya watu, kuna maeneo wanatozwa mpaka laki mbili mpaka laki tatu kwa mwaka ni gharama kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunategemea hizi Kanuni zinapokuja Bungeni ,kwa sababu Bunge imekasimu madaraka kwa Wizara lazima Kamati hii ya Sheria Ndogo ihakikishe wanazipitia na kuweza kurudisha mrejesho kwa Serikali ili ziweze kufanyiwa marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umuhimu wa sheria hii kama chombo hiki kitakuwa hakina bajeti ya kutosha sheria hii nayo itakuwa haina nguvu ya kufanya kazi. Gharama za vifaa vya zimamoto ni kubwa sana, kuna gari inauzwa mpaka bilioni mbili gari moja ya zimamoto. Kwa hiyo, upo umuhimu wa Serikali kutazama ni namna gani wanaweza kusaidia kuilea na kulibeba Jeshi hili ili liweze kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna mambo mengine lazima tuwe wazi tufunguke, Ujerumani State of Hamburg walishatoa offer kujenga Fire Academy hapa Tanzania na Academy hiyo haipo popote South of Sahara, tungeweza kupata wanafunzi kutoka maeneo mengi sana nchi jirani na sisi maeneo haya kuja kujifundisha na Serikali ingeweza kupata mapato makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, vitu kama hivi vikija vinakaliwa havifanyiwi kazi, kwa hiyo utakuta watu hawana appetite ya kufanya kazi sijui kwa sababu gani.

Kwa hiyo, naomba nitoe rai tu kwa Waziri na timu yake offer kama hizi zikija, kuna offer ya pale Mchicha - TAZARA Serikali ya Japan walitoa tu condition jengeni jengo tutawaletea magari, tutawaletea training tutawaletea na madawa ya vifaa vya kuzimia moto, mpaka leo lile jengo sasa hivi wamekaa pale vibaka na wahuni ambao wanafanya mambo ambayo siyo, yote haya ni kwa sababu bajeti hakuna. Hivyo, ninaiomba Serikali wajaribu kuwapa kipaumbele kwani moto ni janga ambalo halina hodi.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo na mimi nikushukuru sana kwa namna ulivyotuongoza na namna tunategemea utatuongoza katika siku za mbele.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, agizo la Chama cha Mapinduzi kwa Serikali kutaka uchumi uwe asilimia nane unaweza kufanikiwa katika Taifa letu ikiwa ni pamoja na asilimia za juu zaidi. Ili kufikia hapo ni lazima Benki Kuu ya Tanzania iwe ina-regulate (inasimamia) riba kwenye mabenki ya biashara nchini mwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, riba za mabenki ni kubwa mno, ili kukuza uchumi ni lazima riba zishuke. Riba zikishuka zitafanya vilevile na kodi kwa upande wa TRA ambapo sasa hivi wanakusanya kodi vizuri, wanaweza kukusanya zaidi wakiwa na kodi rafiki. Kodi rafiki itamwezesha mlaji au private sector kuwa na mishahara mizuri kwa watumishi wao. Ukiwa na mishahara mizuri nominal wages ikiwa above inflation rate mlaji anakuwa na disposable economy. Disposable economy TRA watapata kodi kutoka kodi ya ulaji ambayo mteja wake atakuwa na uwezo wa kwenda kununua bidhaa katika soko ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe TRA pamoja na kazi nzuri wanayoifanya, wajaribu kuwa na kodi Rafiki. Kwa takwimu za TRA walipaji kodi Tanzania ni wachache sana, tuwe na wigo mkubwa wa walipaji kodi na kodi ikiwa rafiki lazima TRA watapata kiwango kikubwa sana cha ukusanyaji kodi na itaendana sawasawa na pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi rafiki inachangamsha biashara ndani ya nchi. Leo shughuli za za biashara Kariakoo asilimia kubwa zimelala kwa sababu ya kodi za TRA wanazoziweka siyo rafiki. Wakiweza kubadilika kuweka kodi rafiki wataweza kuwafikia wateja wengi na wateja wengi wakilipa volume ya kodi itakuwa kubwa na kuifanya TRA iweze kukusanya mapato kwa rekodi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inajenga barabara kwa pesa za ndani, ni jambo nzuri sana. Daraja la Kigamboni ni mfano mzuri wa PPP kati ya Serikali na private sector. Leo Daraja la Kigamboni linakusanya shilingi 1,100,000,000 kwa mwezi takribani shilingi 13,000,000,000 kwa mwaka. Kwa hiyo, inaelekea kwa miaka 15 ijayo deni la uwekezaji wa Daraja la Kigamboni litakuwa limekwisha. Maana yangu nini? Serikali na wataalam wa TRA wawe sasa na muono wa kutazama road toll kugharamia barabara ambazo zitakuwa zinatumika ili fedha hizi ziweze kutumika kujenga barabara zetu za ndani na za mikoani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mijini katikati barabara zinajengwa na TARURA lakini barabara hizi bado zinakuwa na msongamano kwenye barabara za TANROADS kwa sababu barabara za mijini hazina uwezo wa kubeba magari haya. Wakiweza kutengeneza barabara za ndani au za mitaani zitaweza kusaidia barabara zinazounganisha Mikoa na Wilaya kuweza kupitika kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali watizame namna gani road toll itakavyoweza kusaidia kujenga barabara ndani ya nchi yetu. Kwa kufanya hivyo, tutaipunguzia Serikali mzigo kwa sababu pesa nyingi za ndani zinaweza zikatumika kuwekeza kwenye kilimo, elimu na kwenye mambo mengine sana ya tafiti ambayo ni muhimu kwenye Taifa letu. Barabara za ndani ambazo ndiyo zinabeba mazao ya wakulima zitaweza kuwa zinapitika ikiwa barabara kubwa zitajengwa kwa njia ya road toll. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali pamoja na mikakati mizuri inayoendelea kufanywa tufungue wigo wa kuongeza walipa kodi. Walipa kodi waliokuwepo sasa hivi wanalipa kodi vizuri na sasa hivi kutokana mwamko wa Serikali yetu hii ya Awamu ya Tano wafanyabiashara wote wana- appetite ya kulipa kodi, wako tayari kulipa kodi, lakini kodi yenyewe walipe wengi wasilipe wachache ili kufikia target ya Serikali. Nina uhakika kama tukiwa na kodi rafiki, makusanyo ya Tanzania yatazidi asilimia 30 ya pato la Serikali na yakizidi maana yake Serikali itakuwa na uwezo wa kujiendesha na itajipa heshima kubwa sana ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango wa kununua ndege ya mizigo. Naiomba Serikali, ndege za mizigo ni jambo muhimu sana kwa ajili ya kusafirisha bidhaa zetu kuzitoa hapa na kuzipeleka kwenye masoko. Ndege hii isifanye kazi tu ya kupeleka bidhaa zetu kwenye masoko ya nje ifanye vilevile kazi ya kubeba mizigo yetu ndani ya soko la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo ndege itakayonunuliwa lazima iweze kukidhi malengo haya yaani iwe ndege kubwa lakini iweze vilevile kutua kwenye viwanja vidogo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Umeniwekea dakika kumi Mheshimiwa?

MWENYEKITI: Ahsante sana tayari.

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Waheshimiwa Wabunge wenzangu tumeondokewa na Rais mpendwa Mungu amuweke pema, mwanamme mashine. Tumempata mwanamke mashine Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tumpe nguvu, tumuombee dua atimize majukumu yake. Mheshimiwa Rais Samia ameshaanza kuonesha mwanga kufuata nyayo za Mheshimiwa Magufuli, tumsaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Afrika lazima iamke kwenye natural resources ambazo Mungu ametupa katika Bara hili la Afrika. Ripoti ya Umoja wa Mataifa inasema the enclave nature of mining industry can limit the trickle down of benefit unless sovereign government participate fully in managing extract industries, kitu ambacho mara nyingi nchi za Afrika na sisi vilevile bado hatujafikia kiwango kizuri cha ku-manage migodi yetu na natural resources ambazo tunazo. Pamoja na marekebisho ya sheria tuliyofanya ambayo tunapata 16% lakini bado tuna haki ya kumiliki migodi hii kwa 100%, kwa kufanya sisi wenyewe kazi ya ku-extract industries za migodi nchini mwetu Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya kuchunguza madini ya almasi na tumeona wawekezaji wa madini haya hawana ujanja mwingine wowote zaidi ya kutumia madini haya kama dhamana. Serikali yetu inaweza na wao tukatumia madini yetu haya yawe dhamana ya kupatia mtaji na hawa wataalamu tukawakodisha na tukawaajiri na wakawa wafanyakazi wa Serikali. Ni hatari kubwa sana kuacha mali hizi zinaondoka wakati sisi Tanzania hatupati market value ya extract industry ya mining katika nchi yetu. Tunapata pesa kidogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo dhahabu ni zaidi ya Dola 2,000 tujiulize katika hizo Tanzania tunapata ngapi? Tunachokipata ni kidogo sana, lazima tubadilike na sasa tu- run sisi wenyewe migodi hii. Najua kuna cartel kubwa sana ya multinational companies kutotaka nchi za kiafrika kuendeleza migodi yao wenyewe. Wanataka lazima waje wao wadanganye kwenye masuala ya mengi sana hasa kwenye operation cost.

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima Serikali, najua kuna vitengo katika idara zote ambazo zinaangalia operation cost waongeze umakini na ujuzi. Katika Mgodi wa Mwadui tuligundua mtambo unaandikwa dola milioni 8 kumbe mtambo umenunuliwa kwa shilingi milioni 5 Tanzania hapa hapa. Kwa hiyo, vitu kama hivi vinaongeza operation cost kuwa kubwa na kufanya faida ya Serikali kupungua, lazima tuamke. Pia lazima tuwe na sehemu ya National Revenue Management Schemes such as Stabilizing Funds inflected cost of projects. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tuhakikishe mali ya Tanzania na Afrika kwa ujumla inalindwa na inaendeshwa na Watanzania wenyewe. Siri kubwa ni kuweka dhamana migodi tufanye wenyewe, tusiwape wawekezaji, wao waje na teknolojia tuikodishe, tuwalipe mishahara wabaki kama wafanyakazi wa kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye ATC inajitahidi kutoa huduma na kufanya kazi vizuri. ATC haiwezi kupata faida au kujiendesha kwa ununuzi wa ticket. ATC kama ni national carrier lazima Serikali iwapunguzie baadhi ya operating cost. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndege ya Shirika la Ethiopia hailipi landing fee, parking fee, navigation fee, hailipi gharama nyingi sana wanapunguziwa au kufutiwa ili kuwasaidia wakue. Sasa ATC ina gharamia gharama zote hizi, inafanya kupunguza mapato yao. ATC hii mpya chini ya Mheshimiwa Matindi, 100% mishahara ilikuwa inalipwa na Serikali leo Serikali inatoa only 17%, inaonesha wanaanza kuja na wakianza kusaidiwa watakuwa vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndege hazitakiwi kukaa chini ya ardhi, anayepumzika ni rubani na crew, ndege inaruka twenty-four seven. Sasa kama hatuna viwanja vyenye ubora wa ndege kuruka usiku, Serikali lazima iwekeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Dodoma zimewekwa taa intensity yake haiwi-controlled na Control Tower ambapo siyo jambo la kawaida. Hii inaweza ikaleta madhara wakati wa giza nene taa zisiweze kuwaka vizuri kama Control Tower hawawezi ku-control intensity ya taa zile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi naomba tuboreshe viwanja vyetu, hapa Dodoma waweke Vertical Approach Slop Indicators (VASI) na ILS ambayo inasaidia hata kwenye mawingu ndege zinatua. Mara nyingi tu ndege za ATC zinarudi sababu zinashindwa kutua. ILS ni chombo ambacho kinaleta usalama kwa abiria, kwenye kiwanja na kwenye ndege. Uwanja wetu huu sasa hivi unapitiwa na watu wengi sana lazima tuboreshe viwanja vyetu kuwe na usalama wa hili shirika letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kuhusu mradi wa DMDP, Mkoa wa Dar es Salaam. Naomba Serikali iendelee kufanya maamuzi, Dar es Salaam 2025 itakuwa na population ya watu milioni 10. Deni lolote ambalo Serikali imelikopa kwa niaba ya Mkoa wa Dar es Salaam linalipika kwa michango na uchumi ambao Dar es Salaam wanao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine huu ni mwezi wa Ramadhan tende jamani siyo chakula cha Waislamu, tende ni chakula alikula Yesu Kristo na katika vyakula alivyopenda Yesu Kristo ilikuwa tende na mkate wa mana. Ukisoma Wagalatia 5:22-23, chakula cha kwanza ambacho kina spirit tende imetajwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi sababu Waislamu wako katika mfungo na tende hizi ni sadaka, Serikali ifikirie kutoa ushuru wa tende ili wananchi wa dini zote waweze kula tende. Wakristo wale tende sababu Yesu kala, Waislamu wale tende sababu Mtume Muhammad naye amekula. Kwa sisi Waislamu ni suna na kwa Wakristo ni suna. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mkisema Waziri haruhusiwi kubadilisha sheria tumeanzisha mtindo wa force account. Force account ni uwekezaji au utendaji wa kazi unaofanywa bila kulipa VAT. Kwa hiyo, tende nazo vilevile Waziri aseme tu tunaruhusu, itoke executive order tende ziruhusiwe bila ushuru tupate kula tende, tupate kufuata suna za Mitume wetu waliopita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na tende hizo ukitizama wana wa Israel walivyotoka kwa farao walivyoingia jangwani ukisoma Exodus 15:27 chakula chao cha kwanza ni tende. Kwa hiyo, naomba Serikali ili nchi iendelee kuwa na neema ruhusuni tende bila ushuru ili Waislamu na Wakristo tule tuweze kupata neema za Mwenyezi Mungu. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye suala la wafanyabiashara, Serikali mmekaa sana na wafanyabiashara…

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga, ahsante sana.

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nakushukuru nichukue nafasi hii kwanza kumpa pongeza kwa kupata nafasi hii nzito, lakini tunaamini Mwenyezi Mungu atamuongoza na atamsaidia katika kazi zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri kwa vile umeingia sasa wataalam halmashauri zetu nikisema wa nchi nzima wanahitaji wapewe training, training za innovation, training za teknolojia, training ambazo wataifanya Tanzania iweze ku-score zaidi kwenye human development index tunaboresha huduma za afya tunaboresha huduma za elimu lakini lazima kuwe na training za ziada ili waweze kufanyakazi vizuri na kuivusha nchi hii iwe sasa iende katika kutambulika katika HDI.

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam jipya yeye pamoja na Madiwani wa Jiji la Dar es Salaam kwa kazi nzuri wanayoifanya na kuweza kukusanya mapato kwa 98% kwa mwaka takriban billion 60. Hakuna halmashauri yoyote katika nchi hii inayokusanya bilioni 60 kwa mwaka kama Jiji jipya la Dar es Salaam la Ilala ambalo lina Majimbo matatu ya Segerea, Ilala na Ukonga.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jiji hili bado barabara zetu ni mbaya nimesema kwenye swali lile la muda uliopita sitaki kuchukua muda mwingi kwenye suala la barabara. Tunalo tatizo kubwa sana tumerudishiwa kukusanya property tax, property tax hii tunarudishiwa kukusanya si mali yetu tunakusanya lakini mapato haya yanakwenda Serikali Kuu ambalo ni jambo zuri lakini gharama za kukusanya hatulipwi kuna running cost za mafuta, kuna running cost manpower, kuna running cost hela nyingi sana ambazo tunatakiwa tuzipate nimuombe Mheshimiwa Waziri hili alitazame ili tuweze kulipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo jiji lilivyovunjwa halmashauri ya Manispaa ya Ilala ilikabidhiwa miradi yote na mali zote za Jiji la Dar es Salaam ambazo ziko katika paramita za Jiji jipya la Dar es Salaam parking fee ambayo ni halali ya kukusanywa na Jiji la Dar es Salaam tunagombania na TARURA, TARURA wanataka na sisi tunataka nikuombe tu Mheshimiwa Waziri uone umuhimu TARURA wakichukua hizi pesa hawazirudishi kuboresha hizi barabara. Kwa vile hawaboreshi barabara ni bora tuzikusanye sisi ili tuwape watengeneze barabara za Mkoa mpya wa Dar es Salaam kwa maeneo ambayo pesa hizi zinakusanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri ulitazame hili na mapambano ambayo tunapambana sasa hivi katika Jiji la Dar es Salaam kuhusu mapato. Mapato ya Jiji la Dar es Salaam Jipya kwa mwezi kwenye fee ya parking 1.1 billion shillings ni hela nyingi sana. Sasa hii ni halali ya wakazi wa Dar es Salaam si halali ya TARURA.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nikuombe lingine TARURA wanafanyakazi vizuri sana wana wataalamu wazuri CO wao mzuri ma-engineer wazuri lakini hawana pesa. Pesa wanazopewa na Serikali wanapewa pesa za maintenance. hawapewi pesa za kutengeneza barabara nimeona kwenye vitabu sasa hivi kuna pesa zimetoka za maendeleo. Lakini naomba u-revisit na Hayati Rais Magufuli alitoa agizo siku alipokuja kufungua soko la Kisutu Jiji jipya la Dar es Salaam lipewe pesa zaidi za barabara ili uchumi ukue na tuweze kusaidia maeneo mengine nje ya Mkoa wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri pamoja na Serikali kwa ujumla, Waziri wa Fedha yuko hapa, fee ya ada ya simu, miaka yote tunapigania mapato ya simu, Ethiopia miradi mikubwa inaendeshwa na ada na tozo katika simu. Tukitoza shilingi 50 tuna-card holders wa simcard Tanzania sasa hivi zaidi ya milioni 52, tuchukue watu wachache milioni 30; only thirty milioni wale ambao wataweza kulipa shilingi 50 kwa siku we end up getting bilioni 540. Tutafute vyanzo vipya, TRA msidumae tu kukamata Bharesa, Mohamed Dewji, sijui Enterprises nani, tafuteni vyanzo vipya, there is a lot money kwenye simu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitizama hii sintofahamu ya bando ambapo tumechukua kama mwezi mzima au wiki tatu fedha zimepotea. Hebu TCRA fanyeni forensic audit kwenye evarage users per kila mtu mtizame shilingi ngapi ambazo makampuni hayo yamechukua ili muweze kuwadai zirudi katika Mfuko wa Serikali na zilete maendeleo katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe masuala ya wananchi kulipa ada ya ziada ya simu ni uzalendo. Leo hatuandiki barua, hatuna gharama ya stamp, leo mtu yuko Mwanza anauliza soko la Pugu la ng’ombe ni shilingi ngapi, leo mtu yuko Mwanza anauliza soko la samaki ni shilingi ngapi, hii ni nafasi nzuri tuwe na kodi ya uzalendo. Tukisema shilingi 50 kwa watu milioni 30 tunaenda kupata bilioni 540. Tukisema tukiweka shilingi 100 kwa siku tunapata trilioni moja na bilioni themanini. Haya ni mapato ambayo yatasaidia kuchochea maendeleo ya nchi yetu na maendeleo ya Dar es Salaam na majimbo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali lazima ije sasa na mikakati ya kuboresha miundombinu. Nimeuliza swali hapa lakini naendelea kusisitiza kwa vile nina muda umuhimu wa kuboresha miundombinu ya Mkoa wa Dar es Salaam. Kibamba, Ukonga, Ilala, Segerea miundombinu ni mibovu, kuna maeneo hayapitiki katikati mjini. Leo tumeoneshwa wabunifu ambao wameshinda tuzo za Afrika, wanapokuja kupewa hizi zawadi, wale wanaokuja na hizi zawadi wanashangaa barabara za wabunifu Tanzania. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Serikali ione umuhimu wa kuboresha miundombinu hii. Fedha zipo, tubadilishe aina na namna gani ya kutafuta kodi za Watanzania. Fedha ziko nyingi sana tubadilishe mfumo wa kukusanya kodi ili sasa mapato haya yaweze kupatikana kwa wingi sana na yaweze kusaidia Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa DMDP II, ni mradi muhimu sana kwa Taifa na kwa Dar es Salaam. Mradi huu haupo Dar es Salaam tu, uko nchi nzima. Dar es Salaam inatajwa sana kwa sababu kwa sababu ni D inaanza na Dar es Salaam na mradi huu upo kwenye umwagiliaji, Kilimo, kuboresha masuala mengine ya utalii na vitu vingine. Kwa hiyo, naomba sana tuendelee kuboresha miundombinu tupate maendeleo katika Taifa letu. Tuboreshe Dar es Salaam, tuijenge Dar es Salaam ili iweze kusaidia mikoa mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, biashara Dar es Salaam zimekufa, wafanyabiashara wa Dar es Salaam wanaondoka wanakwenda nchi zingine kufanya biashara sababu wanashindwa kupita kwenye barabara katikati ya mji. Jimbo la Ilala lina wakazi wengi wanasema wa chache ni kweli lakini kuanzia asubuhi saa kumi na moja mpaka saa tatu usiku tunaudumia watu milioni mbili katika kieneo kile, utaona uchumi ambao unaweza ukawa generated kwa watu wale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pengine nimkumbushe Mheshimiwa Waziri a-train watu wake katika innovation na teknolojia mpya waweze kuwa na uelewa mkubwa kwenye mambo ya afya, elimu na katika mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Kamati yetu hii, na kunipa nafasi ya kwanza.

Mheshimiwa Spika, mimi nipo kwenye Kamati hii toka mwaka 2005 nilikuwa Makamu Mwenyekiti wakati wa Mama Anna Abdallah, Makamu Mwenyekiti kipindi cha Masilingi, Makamu Mwenyekiti kipindi cha Lowassa na Mungu amenijalia sasa kwa rehema zake na mapenzi yake nimekuwa Mwenyekiti wa Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ni pesa za maendeleo ambazo zinatakiwa zije kwenye Wizara hii haziji. Tunatatizo kubwa sana za kutumia pesa kulipa pango katika mabalozi nje ya nchi, takribani kwa miaka kumi Serikali inatumia siyo chini ya shilingi bilioni 220 kulipa pango tu, pesa hizi zingeweza kuwa re-invested na tukawa tuna majengo yetu na ikawa ni heshima kwa Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiwa na majengo yetu tuna nafasi ya kupata kodi na tuna nafasi ya kutokulipa kodi kwa nchi zingine, sijui kwa nini hii hoja Serikali wanaiona ni nzito kwao. Mwaka 2021 na tumeitoa kwenye taarifa pesa za maendeleo shilingi bilioni 20 hata senti tano mpaka leo haijatoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeahidiwa kwenye kikao cha pamoja kwa mujibu wa kanuni zetu, Kamati ya Uongozi na Kamati ya Bajeti kwamba fedha zitalipwa by May na sina taarifa mpaka sasa hivi kama hizo fedha zimelipwa. Ni jambo ambalo linaturudisha nyuma. Kuishi katika nyumba za kupanga Balozi wa Tanzania ni kutoku-secure information za nchi huko tuliko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, usalama wa taarifa za Balozi na makao makuu ya nchi unakuwa na mashaka makubwa. Tulipangiwa mwaka 2019/2020 bilioni nne; fedha zilizotoka ni takribani milioni 300 tu. Sasa bila kuwa na fedha zetu au bila kuwa na majengo yetu hatuwezi kuwa na diplomasia nzuri ya uchumi. (Makofi)

Hoja yangu kubwa na Waziri wa Fedha yuko hapa, niombe waweke uzito mkubwa sana wa namna gani kuisaidia Wizara hii iweze kupata fedha za maendeleo. Tumeweza kununua nyumba New York naipongeza Serikali, nyumba ile sasa nayo tunakaa wenyewe bila kulipa kodi, lakini vilevile sasa tunatoza watu kodi kwa kuwapangisha katika eneo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna kiwanja Uingereza primed area, huu zaidi ya mwaka wa 15 mpaka kiwanja kile sasa kinaota magugu. Kuna gharama kubwa ya kutoa ile mizizi na inakuwa ni aibu na mpaka sasa mwisho, majirani kwenye kiwanja kile wanalalamikia kwenye Serikali yao, kiwanja kile tunyang’anywe na kiwe mali ya Serikali ya Uingereza na sisi tukose. Yote hatupeleki fedha za kujenga majengo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mengi tunayasema kwenye ripoti yetu sitaki kuingia kwenye mambo mengi sana niwaachie wajumbe wengine, lakini mimi nilitaka kujenga hoja kwenye nyumba tu, tuweze kununua nyumba zetu, tumiliki nyumba zetu na tuzikarabati ziwe mali ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashindwa sasa hivi mpaka na mataifa mengine madogo namna wanavyokuwa na majengo. Kuna nchi hapa Afrika Mashariki ukienda pale Mtaa wa UN, unaona jina lake inapendeza kuona pale House of Uganda. Kwa hiyo, mimi niombe sana Serikali, Waziri wa Fedha uko hapa, Chief Whip yuko hapa, tunaomba Wizara hii muipe fedha iweze kukarabati na muwape fedha ili tuweze kununua tumiliki nyumba katika nchi za mabalozi yetu nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
THE WRITTEN LAWS (MISCELLANEOUS AMENDMENTS) (NO. 5) ACT, 2021
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Siku ya Ijumaa inayokuja panapo majaliwa, Kamati ya Ulinzi na Usalama itakuletea Azimio la Kupambana na Ugaidi na protocals ambazo Tanzania imeridhia, sasa Bunge lako itabidi likubali kuridhia ili sasa nasi tuwe katika signatory wa Bara ya AU pamoja na Umoja wa Mataifa.

Mheshimiwa Spika, katika commitment za States zipo 12; (b) inasema: “prevent the entry into the training of terrorist groups on their territories.” Response ya kwanza ya nchi ya ku-prevent wahamiaji haramu, ku-prevent wakimbizi haramu, wanaotembea na silaha ni uhamiaji. Ndio wa kwanza, hakuna popote pengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, chombo hiki cha Uhamiaji sasa hivi ninavyosema, kipo kwenye theatre for operation, kwenye vita Msumbiji kinapambana na magaidi wa Msumbiji, chombo hiki ambacho kinasimamiwa na Jenerali wetu makini kabisa General Anna Makakala. Sasa watu na amani hii mnayoiona Tanzania ni sababu ya vyombo hivi ambavyo vinafanya kazi. Nchi yoyote lazima iwe na msemo, nasi Tanzania tunasema, “Uniting and Straightening Tanzania by providing appropriate tools required to intercept obstruct malicious activities within our borders by arming our enforcers.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ukienda Marekani kuna Transport Security Agency, wale wote ni watu wa Uhamiaji. Sasa inawezekana wengine hawajui. Ukienda Dubai, zamani walikuwa wanavaa uniform, sasa hawavai uniform, lakini vitu wanavyo chini ya meza. Akiingia mhalifu, wanapambana naye. Vile vile, kwa mara ya kwanza katika Taifa letu, Amiri Jeshi Mkuu ndiye aliyemteua Kamishna General wa Uhamiaji na ndiye aliyemwapisha na kumvisha nyota hadharani cheo chake kwa kuonesha sasa hawa ni Jeshi. Kama alivyosema Mheshimiwa Dkt. Pindi Chana, tumechelewa kuleta hii sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiki ni chombo muhimu katika vyombo vyote vya jeshi. Response ya kwanza kwenye mipaka ni wao, hakuna chombo chochote kingine. Tunapotaka kuweka vigezo kutoku-strengthen amani ya nchi yetu kwa kutumia Katiba we are wrong somewhere. Tunapovamiwa kwenye mipaka, tunapovamiwa nchini, hakuna Katiba itakwenda kusimamisha hayo mapigano ya hao wanaokuja kuleta Tanzania, bali ni vyombo hivi ambavyo vipo chini ya Amiri Jeshi Mkuu wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba wenzangu waelewe umuhimu wa vyombo hivi, wana uwezo wa kijeshi kupambana na uhalifu wowote malicious yote ya attack ambayo itataka kuja hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana tena sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Muda wangu ulikuwa mdogo, lakini nilitaka niguse hapa hapa kuwasaidia wenzetu waelewe umuhimu wa chombo hiki.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, ahsante sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)