Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Cecilia Daniel Paresso (52 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja iliyoko mezani. Nianze kwa kusema Serikali nyingi duniani huongozwa kwa Katiba iliyojiwekea, Sheria zilizopo, Kanuni zilizopo, Taratibu zilizopo au Dira
ambayo imejiwekea kama nchi, lakini katika Serikali ya Awamu ya Tano tunaona mnaongozwa
kwa kauli mbiu ya hapa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mtanielewa tu! Nasema mnaongozwa kwa hapa kazi, bila kufuata Sheria zilizopo, Kanuni zilizopo, utaratibu uliopo na Katiba mliyojiwekea. Nasema haya kwa mifano nitakayoitoa; Rais anafukuza watumishi wa umma! Ni kweli kwamba kuna baadhi ya watumishi wa umma sio waaminifu na wana upungufu. Pia, ni kweli kwamba kuna baadhi ya watumishi wako kwenye mamlaka ya Rais, wale aliowateuwa anaweza kuwaondoa, lakini kuna wale ambao wameajiriwa, ni sharti taratibu na sheria za kiutumishi zifuatwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine; mmesema mnatoa elimu bure, mtapeleka takribani shilingi bilioni 18 kwa Halmashauri! Mnapeleka kwa bajeti ipi ambayo hatujapitisha ndani ya Bunge? Bunge la Kumi, tulipitisha Bajeti, ni lini mmeleta Supplementary Budget ndani
ya Bunge, ili mtekeleze hili? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine, Rais alifuta sherehe za Uhuru! Ni kweli kwamba katika Bunge la Kumi kati ya mambo ambayo Upinzani tulikuwa tunapigia kelele, ni kufuta sherehe mbalimbali ambazo hazina tija, ni jambo jema. Amefuta sherehe za Uhuru akatoa agizo fedha zipelekwe kwenye ujenzi wa barabara ya Morocco; amefanya fedha hizo zimekwenda, taratibu za manunuzi, kutangaza tender, Sheria mliyojiwekea ya Manunuzi, mmefuata au mnasema tu hapa kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, kupitia vyombo vya habari, jana au juzi, Afisa mmoja wa Serikali amesema watapeleka shilingi milioni 50 kwa kila kijiji! Nawauliza kwa Bajeti ipi? Kwa Sheria ipi? Kwa Supplemantary Budget ipi mliyojiwekea? Au mnaongozwa tu kwa hapa
kazi, bila kufuata sheria zilizopo? Mtakuwa ni Serikali ya ajabu duniani kuongozwa na kauli mbiu badala ya sheria mlizojiwekea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Hotuba ya Rais ameelezea kwa upana suala la amani na utulivu na mmekuwa mkijivunia amani na utulivu. Mnawaambia Watanzania kuna amani na utulivu, wakati hakuna demokrasia ndani ya nchi hii, demokrasia zinaminywa zinakanyagwa.
Kuna migogoro ya ardhi, wakulima na wafugaji, halafu mnasema amani na utulivu! Hakuna ajira kwa vijana, halafu mnasema amani na utulivu! Mahakama hazitoi haki kwa wakati, halafu mnasema amani na utulivu! Hospitalini hakuna dawa, kinamama wakienda kupata huduma
zipo mbali au wakati mwingine hazipatikani, mnasema amani na utulivu! Tumeona utumiaji wa nguvu za kidola wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi, halafu mnasema amani na utulivu!
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, itafika mahali Watanzania hawatathubutu tena kuvumilia amani na utulivu wakati wana shida lukuki! Hakuna haki, watu wanakandamizwa, watu wananyanyaswa, halafu mnang‟ang‟ania kusema amani na utulivu! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie machache kwa kusema katika Hotuba ya Mheshimiwa Rais, ameelezea hali ya kisiasa Zanzibar. Hili tunamwambia nalo ni jipu alitumbue, alifanyie kazi! Mshindi atangazwe! Si mmesema ninyi hapa kazi! Fuateni basi Sheria, Katiba na Taratibu mlizojiwekea. Mtangazeni mshindi wa Zanzibar, kwa nini mnaogopa? Mkiambiwa hili mnaogopaogopa na mnaanza kupiga-piga kelele, kuna nini kimejificha hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka suala la mgogoro wa kisiasa, kama amesema yeye atakuwa ni Rais wa kutumbua majibu basi atumbue na hili, Wazanzibari wapate haki yao waliyemchagua aweze kutangazwa. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Mfuko wa TASAF; Fedha hizi ni mkopo toka World Bank kiasi cha dola za Kimarekani 220,000,000 ili kusaidia kaya maskini nchini. Kaya hizo kulingana na utofauti wa mahitaji, hupewa kati ya sh. 20,000 hadi sh. 62,000 kila baada ya miezi miwili.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango huu ni wa miaka mitano, je, Serikali imejipangaje kufanya mradi huu uwe endelevu? Je, Serikali itaweza kugharamia mradi huu pindi muda wa mradi kwisha ukifika?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, Serikali imekuwa na mwenendo wa kuanzisha miradi na Mifuko mingi bila kuwa endelevu na kutoleta tija inayotakiwa. Mfano wa Mifuko iliyoanzishwa ni pamoja na Mabilion ya JK, Mfuko wa Wanawake na Vijana (Halmashauri za Wilaya), TASAF, Mfuko wa Dhamana ya Mikopo, Mfuko wa Amana ya Ubinafsishaji na sasa shilingi milioni 50 kila kijiji. Kwa nini Serikali haioni umuhimu wa kubadili mtindo huu wa kutoa fedha mikononi mwa wananchi kwani kwa kufanya hivyo haiwezi kuondoa umaskini au kuboresha maisha yao, umuhimu ungewekwa kwanza kuboresha huduma muhimu za kijamii kwa kiwango cha juu na ndipo tuwaze mpango huo wa kutoa fedha kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, je, katika Mifuko hiyo tathmini ya kina imefanywa ili kupima matokeo yaliyotarajiwa? Ni kwa kiwango gani Mifuko hiyo imekuwa endelevu? Serikali haioni umuhimu wa kuachia sekta binafsi ifanye na kutekeleza mpango huu na Serikali ibaki kama mdhibiti? Nashauri Serikali ijipime upya na kuacha kufanya mambo au maamuzi kwa mazoea.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. CECILIA D. PARESO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwanza naunga mkono maoni yaliyotolewa na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani hapa Bungeni na nafikiri Serikali ni vizuri mkayapitia, mkasoma na mkayachukua kuyafanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano ilipoingia madarakani iliingia kwa mbwembwe nyingi ikijiita ni Serikali ya ‘Hapa Kazi tu.’ Lakini Serikali hii ya ‘Hapa Kazi Tu’ pia kupitia hotuba ya Waziri Mkuu ukurasa wa 11 inasema ili kuboresha demokrasia hapa nchini hatuna budi kujenga jamii inayoheshimu na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu. Wameandika hivi kwenye vitabu lakini sisi Wabunge na wananchi ni mashahidi kwamba hii Serikali ya hapa kazi ndio Serikali ambayo inavunja katiba, inavunja sheria, haifuati taratibu na haifuati misingi ya utawala bora. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivi? Sababu zipo nyingi lakini kutaja tu kwa uchache hoja mojawapo tu, leo tunawadhibiti na kuwanyamazisha wananchi na vijana mbalimbali ambao wanatoa maoni yao kwa namna yoyote katika nchi hii. Tunajenga vijana wawe waoga kwenye nchi yao, tunawaziba midomo vijana na wananchi wasitoe maoni yao wakati katiba ya nchi imetoa uhuru huu kwa wananchi kutoa maoni yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunavinyima vyama vya siasa visifanye mikutano wakati katiba na sheria zinaruhusu; na uhai wa vyama vya siasa, chama chochote cha siasa ni kufanya mikutano ya hadhara, ni kukutana na wanachama wake. Uhai wa wa vyama vya siasa ni kuongeza wanachama kwa sababu hawa wanachama; ni kama ilivyo makanisa kwenye vyama vya siasa, leo mtu yupo chama hiki na kesho
yupo chama hiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji kuendelea kuimarisha vyama vyetu kwa kuongeza wanachama, tunaongeza wanachama kwa kupitia mikutano ya hadhara; lakini Serikali leo inapiga marufuku mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa, inavunja katiba ya nchi iliyojiwekea, inavunja sheria. Sasa ndio tunajiuliza hii ndio hapa kazi kweli ya kuvunja katiba na kuvunja sheria? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini leo watu wanatekwa, wananchi hawana amani; kwenye mitandao sasa hivi ukisoma wananchi wanasema hata nikienda mahali naaga naenda sehemu fulani kwa sababu sijui kama nitarudi salama au nitatekwa. Tumeshuhudia hapa kuna watu wametekwa wamepotea, hawajulikani walipo, hakuna kauli ya Serikali; hatujasikia kauli nzito inatolewa na Serikali, tunajiuliza kama Serikali imekaa kimya je, ndiyo inayohusika na hili jambo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kama na ninyi mngekuwa mnaliona jambo hili kweli linatishia amani ya wananchi mngetoa kauli, hamtoi kauli watu wanatekwa, watu hawajui wanapotelea wapi; hatujui kama kina Ben Sanane haijulikani kama ni wazima au wameshauwawa, haijulikani walipo. Hamuwezi mkajiita hapa kazi tu kwa kufanya hivi vitu; au inawezekana mnajiita hapa kazi kwa kufanya hivyo vitu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Serikali hii kupitia Msajili wa Vyama vya Siasa ilitakiwa ilee hivi vyama vya siasa. Leo mnashabikia ugomvi wa ndani ya Chama cha wananchi (CUF); Serikali imechukua upande ina-support upande mmoja na kuacha upande mwingine. Wakati wanachama wa chama hicho wanawatambua viongozi ikiwemo Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF kama ndio Katibu Mkuu wao,
lakini Msajili wa Vyama vya Siasa badala ya kulea chama hiki na kuhakikisha mgogoro uliopo unatatulika wamechukua upande na wanashabikia upande ule ambao wanaharibu Chama cha Wananchi CUF. Sasa hii ndio hiyo inayoitwa ‘Hapa Kazi Tu’. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Devotha ameeleza hapa asubuhi, hakuna tena ile hadhi ya Ubunge; Mbunge unaonekana si kitu na hasa upande wa upinzani wakati wowote unaweza kuvamiwa nyumbani kwako. Yaani Mbunge ni mtu ambaye anaweza akapotea kwenye nchi hii? Mbunge kama anatakiwa polisi akipewa taarifa ya kwenda kituoni hivi atapotea? Kwa nini tunamchulia Mbunge kama ni mtu ambaye anaweza kupotea? Kwa nini polisi wanatumia madaraka yao vibaya kuwaita Wabunge na kuwataka wakati wowote na kutumia silaha nzito utafikiri Mbunge ni jambazi sugu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima Wabunge tutetee hadhi yetu na ni lazima Wabunge tusimame tutetee hadhi ya mhimili wa Bunge; tukisimama hata mhimili wa Serikali nao utaweza kuona kwamba Bunge lina hadhi yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, madai ya katiba mpya nadhani yapo pale pale, tunahitaji katiba mpya. Rasimu ya katiba mpya ilitengenezwa kwa fedha nyingi za walipa kodi, mmeiweka kapuni, mmeificha na hatusikii tena Serikali ya Awamu ya Tano mkizungumzia suala la katiba mpya.
Watanzania wanahitaji katiba mpya; tunahitaji katiba mpya na tunaitaka katiba mpya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mifuko ya Kuwawezesha Wananchi Kiuchumi. Kumekuwa na mifuko mingi sana, kuna hizo asilimia kumi ambazo zinatengwa kutokana na mapato ya ndani ya Halmashauri. Kumekuwa kuna mifuko mingine kupitia Wizara mbalimbali, ya Vijana, ya Fedha na vitu kama hivyo. Kwa nini isifike mahali sasa mifuko hii ikaunganishwa kuliko kuwa na mifuko mingi ambayo inatoa fedha kidogo ambayo mwisho wa siku hata ukipima ufanisi wa hizo fedha haupo kabisa? Kwa nini tusiwe na mfuko mmoja wa pamoja ambao utatoa mikopo kwa vijana, akinamama na makundi mbalimbali ili kuwawezesha kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ushauri wangu ni kuunganisha hii mifuko na kuufanya mfuko mmoja ili iweze kwenda kutoa mikopo kwa wananchi wetu na kuwaimarisha kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2016/2017 ambayo tunaimalizia mwezi Juni. Bajeti tuliyoipitisha ilikuwa ni ya shilingi trilioni 29.5 lakini mpaka kufikia Februari fedha za maendeleo zilizotolewa kwa Halmashauri na Wizara ni asilimia 35 tu. Sasa asilimia 35 tumebakiza miezi kama miwili kwenda kumaliza mwaka wa fedha; kutakuwa na muujiza gani wa kwenda kukamilisha hizi fedha za maendeleo?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sababu ambazo zinaelezwa na Serikali, kwamba kwa nini wameshindwa kufikisha hiyo wanasema kuna fedha za wafadhili nyingine zimechelewa na nyingine hazijatolewa. Wakati tunapitisha bajeti hapa mwaka jana tulieleza athari ya MCC na wafadhili wengine kujitoa, mkasimama mkatetea sana hoja hii mkasema nyie mnaweza kujitegemea, mapato yenu ni mazuri na leo hizi ndio athari. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine tulikuwa tunaona hizi taarifa Serikali ya Awamu ya Tano mnasema mnakusanya karibu Shilingi trilioni 1.2 kila mwezi. Serikali ya Awamu ya Nne iliyopita ilikuwa inakusanya kati ya bilioni 800 mpaka 900 kila mwezi. Kwa hiyo, ninyi mmejigamba kwamba mnakusanya mapato zaidi kila mwezi halafu siku hizi hata hatuoni hizo taarifa za TRA tena; mnajigamba kwamba mnakusanya vizuri kuliko Serikali iliyopita, lakini mnakusanya zinakwenda wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri zetu zipo taabani hakuna fedha za maendeleo; wenyewe mnasema mpaka Februari fedha zilizokwenda ni asilimia tano tu, zingine zinaenda wapi? Mnakusanya zinakwenda wapi? Mtafikiaje kutekeleza bajeti hii ya Shilingi trilioni 29 wakati fedha zenyewe hazijakwenda?
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine inayotolewa kwamba wananchi hawana uelewa wa walipa kodi, mashine za EFD; ni hoja dhaifu sana ambazo zinatolewa na Serikali. Nadhani mnapaswa kutafakari na kutumia taarifa za wataalam ili muweze kufikia haya malengo ambayo
yanatakiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti inayokuja ya mwaka 2017/2018, mnasema mna bajeti ya Shilingi trilioni 31.6; mimi naomba Watanzania muwashangae kama ambavyo mimi naishangaa hii Serikali. Hii ambayo tunamaliza sasa hivi ni trilioni 29 wakati fedha za maendeleo imefika asilimia 35 halafu hiyo projection ya 2017/2018 ni Shilingi trilioni 31, hivi kuna muujiza? Kuna Yesu atashuka awaletee fedha nyie mkatekeleze hii bajeti? Kwa kweli inashangaza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka Serikali ituambie mnaenda kufanya mabadiliko gani katika ukusanyaji wa kodi au katika kuimarisha kodi ili hiyo bajeti ya trilioni 31 iweze kufikiwa? Mtupe majibu sahihi. Hata hivyo, kama haifikiwi kama ambavyo hii ya sasa hivi tunamaliza
haitafikiwa kwa nini msije na bajeti halisi hata kama itakuwa na kiwango kidogo ambayo inaweza kutekelezeka? Kwa nini mnawafurahisha Watanzania kwa namba kubwa wakati utekelezaji wake unakuwa ni sifuri? Kwa hiyo, tunaomba tuambiwe ni kwa namna gani mnaenda kufanikiwa na bajeti hii. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja ambayo imewasilishwa na Serikali hapa Bungeni. Kwanza naunga mkono maoni ya Kambi ya Upinzani ambayo yamechambua na kutoa mapendekezo mengi. Hapa ndani ya Bunge upande wa pili mmekuwa na mtazamo wa kuona kwamba hatushauri lakini kuna ushauri mwingi sana umetolewa na mapendekezo mengi, naamini Serikali mtaichukua na kuifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kutoa maoni yangu kuhusu utekelezaji wa bajeti ambayo tunaimalizia. Bajeti ya mwaka 2016/2017 tulipitisha shilingi trilioni 29 kama bajeti ya jumla lakini katika hizo shilingi trilioni 29 mpaka tunapoongea ni takribani asilimia 38 tu ya fedha zote ndiyo imeenda kwenye miradi ya maendeleo. Katika fedha hizi za miradi ya maendeleo ambayo Serikali mmepeleka ni kama ifuatavyo kwa ufupi kwa mujibu wa kitabu cha Waziri. Ujenzi na ukarabati wa barabara imepelekwa shilingi bilioni 675, miradi ya uzalishaji wa umeme shilingi bilioni 441, malipo ya awali ya ujenzi wa reli shilingi bilioni 300, usambazaji wa maji vijijini shilingi bilioni 186 na huduma za afya ni shilingi bilioni 170.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunajiuliza hata hizi fedha tu za miradi ya maendeleo ambayo imepelekwa kwa asilimia chache kiasi hiki, zile ambazo ni muhimu kwa afya za Watanzania ikiwemo afya, maji imepelekwa kidogo ukilinganisha na hizo nyingine za ujenzi na ukarabati wa barabara. Kwa hiyo, unaona kabisa hata umuhimu wa kuwapa Watanzania hizi huduma muhimu za maji na afya haupo na wala hazipewi kipaumbele.

Kwa hiyo, Waziri sasa hivi tunaposema hata hii pia hamtaweza kutekeleza tunamaanisha kwa sababu ya maneno yenu ambayo mmeyaandika humu kwenye hivi vitabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii ya 2017/2018 ambayo sasa tunaitarajia kuanza, mnakisia maoteo ya bajeti itakuwa shilingi trilioni 31.7. Kama hii tunayoimaliza ya shilingi trilioni 29 haijatekelezwa hata kwa asilimia hiyo, je, hii tunayoiendea itatekelezwa? Mnawahadaa Watanzania kwa kuwaambia kwamba hii bajeti haijawahi kutokea, ni bajeti ya karne, mimi naamini ni kweli itakuja kuwaumiza Watanznaia kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati mnafanya bajeti hii kufikia shilingi trilioni 31 maana yake bajeti hii ni shirikishi kuanzia Serikali za Mitaa, watu wamepanga kwa mfumo wa O&OD, wakaibua, wakapanga, tukapitisha kwenye Halmashauri zetu, zikapita kwenye process nzima za kibajeti mpaka Serikali mkaja Bungeni mkasema kwamba bajeti ni shilingi trilioni 31. Sasa muone mnavyojikanganya, hii shilingi trilioni 31 ni pamoja na mapato ya ndani ya Serikali za Mitaa kwa sababu bajeti imeanzia kule chini. Halmashauri zetu zimesema zitakusanya ushuru mbalimbali kama mapato ya ndani baadaye mkafanya compilation mkatuletea bajeti ya shilingi trilioni 31 lakini mnatuletea bajeti ya shilingi trilioni 31 huku nyuma mnafuta vyanzo vingi vya Serikali za Mitaa ambavyo tayari mmeshaweka kwenye bajeti yenu. Mheshimiwa Waziri hiki unachokisema shilingi trilioni 31 hautakaa utekeleze kwa sababu umesahau vyanzo vingine umevifuta wakati viko kwenye bajeti ya Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo unatuambia bajeti zimefutwa, kwanza kuanzia miaka ya 2000-2010 Serikali mlifanya maboresho ya Serikali za Mitaa kwa kuziboresha kwa kuweka mfumo ya O&OD, mkasema mnagatua madaraka, mnaziachia Serikali za Mitaa ziwe na madaraka kamili, zikusanye mapato yake, zijiendeshe, leo mmegeuka baadhi ya mapato mnayachukua, mengine mnayafuta bila kuzishirikisha Serikali za Mitaa, hamtambui umuhimu wa Serikali za Mitaa? Mheshimiwa Waziri Serikali za Mitaa ziko kwa mujibu wa Katiba ya nchi kwanza mnavunja hata hii Katiba ya nchi. Leo umekuja unatuambia umefuta ushuru wa huduma (service levy), Halmashauri zetu nyingi jamani zinategemea ushuru wa hizi guest house na zimeshaweka kwenye bajeti yake. Leo unafuta ada ya machinjio, Halmashauri zetu ndiyo zinategemea ipate hizo ada, umefuta ada ya makanyagio minadani Halmashauri nyingi za vijijini ndiyo zinategema hii ada, umeondoa kodi ya mabango umeichukua umepeleka TRA halafu unasema utazirudisha, hamrudishagi mnatudanganya kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnasema mmepunguza ushuru wa mazao kutoka asilimia tano mpaka asilimia mbili kama ni mazao ya chakula na biashara lakini Mheshimiwa Waziri unasahau kwamba Halmashauri zetu tayari zilishaweka fedha hizi kwenye bajeti yao kwa nini mnawadanganya Watanzania? Halafu nitashangaa sana Waheshimiwa Wabunge wa CCM mkiendelea kusema mnaunga mkono hoja, Halmashauri zenu mtaona tukianza mwaka wa fedha hazitakuwa na fedha kwa sababu vyanzo vingi vimefutwa na Serikali Kuu na tayari walishaweka kwenye bajeti zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mnaenda kuua Serikali za Mitaa au basi mseme kwamba Serikali za Mitaa hazipo tena, mfanye vitu vyote. Mmekuwa mkiahidi mara zote kwamba mtarudisha hizo fedha na hamjawahi kurudisha. Mheshimiwa Susan Lyimo amesema hapa Kodi ya Majengo tu, mliahidi mtarudisha hamrudishi hata senti tano. Sasa Serikali za Mitaa zitawezaje kwenda kujitegemea na kufanya shughuli zake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie Kodi ya Majengo. Serikali ya Awamu ya Tano mlichukua kodi hii ya majengo mkasema TRA inakusanya. Juzi niliuliza swali la nyongeza hapa Bungeni kwa Mheshimiwa Waziri Simbachawene, nikataka kujua kauli ya Serikali ni majengo yapi hasa ambayo yanatozwa kodi hii kwa sababu kwenye Wilaya zetu mpaka nyumba za tembe, nyumba za udongo zinatozwa kodi hii. Mheshimiwa Simbachawene akanijibu hapa akasema majengo yatakayotozwa kodi ni yale yanayotengeneza faida kwa maana ya nyumba zinazofanya biashara. Mheshimiwa Waziri wa Fedha ukasimama ukaniambia kuwa subiri bajeti yangu tutasoma, sasa hii bajeti yako ukurasa wa 48 inasema hivi; “Serikali itatoza Kodi ya Majengo kwa nyumba zote kwa viwango vitakavyopangwa na Waziri na Fedha na Mipango. Nyumba ambazo hazijafanyiwa uthamini zitatozwa kwa kiwango maalum (flat rate) cha shilingi 10,000 kwa nyumba na shilingi 50,000 kwa nyumba za ghorofa kwa kila ghorofa.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni zile ambazo hazijafanyiwa uthamini, kati ya shilingi 10,000 mpaka shilingi 50,000, acha zile zingine ambazo zitafanyiwa uthamini. Mheshimiwa Waziri hamuoni ninyi wenyewe mnajikangaya kwenye kauli zetu? Mheshimiwa Simbachawene amesema ni zile ambazo zinaingiza faida, akasema unaweza kwenda vijijini ukakuta mtu ana guest house na kadhalika huyo sawa atozwe kodi lakini wewe unasema nyumba zote, maana yake unasema hata za tembe nazo zitozwe kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu mnasema hii ni bajeti ya kuwakomboa Watanzania au kuwanyonya Watanzania? Mnathubutu kusema kwamba hii bajeti haijawahi kutokea ni bajeti ya karne, hii haiwezekani hata kidogo. Nitawaomba sana Waheshimiwa Wabunge wa CCM mkasome tena upya hii bajeti yenu ambayo mnasema eti inaenda kumkomboa Mtanzania wakati siyo kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Road License. Wamepongeza sana hapa Wabunge wenzetu wa upande wa pili lakini tunajiuliza hivi ni Watanzania wangapi kati ya Watanzania milioni 40 ambao wana own magari? Inawezekana ni asilimia tano ya Watanzania wote, sasa asilimia tano ya Watanzania wote hawa leo mmewaondolea Road License ambayo watalipa kwa mwaka, mnasema mnapeleka kodi hii kwenda kutozwa kwa shilingi 40 kwa kila lita moja ya mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunafahamu ukiweka ongezeko lolote kidogo kwenye kila lita ya mafuta nchi hii, kila kitu kinapanda bei. Kwa sababu mafuta yanahusiana moja kwa moja na masuala mengine, utakuta bidhaa zinapanda sokoni, ukisafirisha mazao bei inapanda na kila kitu. Sasa kwa nini tuwaadhibu Watanzania wengine walio wengi ambao hawamiliki vyombo vya moto kwa sababu hawalipii Road License halafu tunawaacha hawa asilimia 5 tu tunawapa msamaha huu wakati itawagharibu Watanzania walio wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Serikali ya Awamu ya Nne ya JK...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu iliyowasilishwa na Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua Tanzania ni nchi ambayo imeingia katika Mfumo wa Vyama Vingi na hayo yametamkwa na yapo katika Katiba yetu. Kama tunatambua Mfumo wa Vyama Vingi, maana yake tunaamini kwamba Serikali inatambua vyama vilivyopo ambavyo vinaunda huo Mfumo wa Vyama Vingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Waziri Mkuu ameeleza kwamba tuko kwenye Mfumo wa Vyama Vingi takriban miaka 23 leo; na vyama hivi vimeendelea kukua kadri miaka inavyoendelea. Serikali ya Awamu ya Tano ilipoingia madarakani inaonesha jitihada kubwa sana za kuua vyama hivi kwa kuvinyima haki yake ya msingi ambayo inapaswa kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema haya? Uwepo wa vyama hivi unatambuliwa na sheria, ufanyaji wa kazi wa vyama hivi umetamkwa katika sheria. Maana yake Vyama vya Siasa vinatakiwa viendelee kufanya kazi ya siasa kwa kuhakikisha vinaendelea kupata wanachama kadri inavyowezekana na kadri ambavyo miaka inazidi kwenda. Haya yamesemwa na Waziri Mkuu katika hotuba yake ukurasa wa 10, amesema:

“Katika kipindi hiki tumeona ushiriki wa Watanzania katika siasa ukiendelea kuongezeka na uhuru wa kujiunga na vyama vya siasa umeendelea.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unajiuliza, kama Vyama vya Siasa ili viendelee kupata wanachama, maana yake ni lazima vifanye mikutano ya hadhara kunadi na kueleza sera zake, ndivyo ambavyo mwananchi ataamua sasa ajiunge na chama hiki au aende chama hiki au asiwe na chama mpaka pale ambapo ataweza kuridhika kuamua kujiunga na chama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naeleza kwamba ili Mheshimiwa Waziri Mkuu tukuelewe kwenye kauli hii kwamba vyama hivi vinaendelea kufanya kazi yake, halafu huku mmebana uwepo wa mikutano ya hadhara, ni kwa uhakika mnalidanganya Taifa hili na mnawadanganya Watanzania. Utaendeleaje kupima kwamba Chama cha Siasa kinakua kama hakifanyi mikutano ya hadhara ikaongeza wanachama? Vyama vya siasa ni kama Makanisa leo mtu anajiunga, kesho anatoka. Ndivyo hivyo.

T A A R I F A . . .

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu wanisikilize vizuri, naongelea Vyama vya Siasa. Siongelei Mbunge wala Diwani. Kwa hiyo Mheshimiwa Vuma naomba unisikilize vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama mnakataza Vyama vya Siasa visifanye mikutano ya hadhara, hamwezi leo kuja hapa Bungeni na kutuambia kwamba vyama hivi vimeendelea kufanya vizuri miaka 26 iliyopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma, waasisi wa nchi hii walituaminisha Watanzania kwamba tuna maadui watatu wa nchi hii; umasikini, ujinga na maradhi. Kwa yanayoendelea leo, jambo lingine limeongezeka kwa Serikali iliyopo madarakani, adui mwingine ni Vyama vya Siasa. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema haya? Kwa sababu leo tunashuhudia Waheshimiwa Wabunge mbalimbali na Madiwani mbalimbali kila siku ama wanaripoti Polisi au wanakamatwa wanaingia Polisi, wanakaa ndani, waliowaweka ndani wakiridhika kwamba sasa wamekaa ndani kwa muda, wanaachiliwa wanaendelea. Kila leo, ama kuripoti Polisi au kwenda Mahakamani. Hapa tuna Wabunge wengi wana kesi kila kukicha, wanahudhuria Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba Vyama vya Siasa vya Upinzani ni adui mwingine ambaye mmemwongeza. Kwa nini nasema haya? Tumeshuhudia pia kwenye chaguzi ndogo zilizofanyika za marudio, kwanza tumefanya Uchaguzi Mkuu 2015, wananchi wameamua kwa ridhaa yao kuchagua mwakilishi wa chama chochote ambacho walikipenda kwa wakati huo na wakawaweka madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani tuna Wabunge wanaotokana na CCM, tuna Wabunge waaotokana na CHADEMA, tuna Wabunge wanaotokana na CUF, tuna Wabunge pia wa NCCR na ACT. Ni ridhaa ya wananchi kwenye maeneo yao wakawachagua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kiongozi mmojawapo wa CCM anazunguka kuwarubuni na kuwanunua baadhi ya viongozi na Wawakilishi hao ambao wamechaguliwa na wananchi, wanasema wanaunga jitihada wanaingia upande wa pili labda inawezekana ikawa ni haki yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba hawa ambao wanarudi upande wa pili inatulazimu kurudi kwenye uchaguzi. Hapa Bungeni tulipitisha shilingi bilioni 4.7 kwa ajili ya Tume ya Taifa Uchaguzi kwa uchaguzi wa dharura endapo itatokea Mwakilishi yeyote amefariki au kwa namna yoyote ameacha nafasi ile. Leo baada ya hizi chaguzi ndogo, tumetumia shilingi bilioni 6.9.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajiuliza, hivi tunafanya kazi ya kurubuni na kununua wahame upande wa pili; tunarudi tena kutumia fedha za walipa kodi kwenda tena kufanya uchaguzi, huku kuna Watanzania wengi ambao hawana huduma muhimu za kimsingi za kijami! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajiuliza…

T A A R I F A . . .

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachozungumzia hapa ni bajeti tunayoitumia bila ulazima wowote. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ulinde muda wangu, naomba unilinde ninapochangia. Kama kuna Mbunge anataka kunijibu, asubiri akipata nafasi na yeye ajibu ninayoyasema. Halafu najiuliza, haya ninayochangia hapa, kama hamjayafanya kwa nini mnahangaika, si msubiri niseme? Kwa nini mnahangaika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu hapa ni utumiaji mbovu wa fedha za wananchi. Kama tulitenga fedha za dharura endapo kutatokea chaguzi, shilingi bilioni nne, leo tumetumia shiligi bilioni 6.9, kwa nini tusingefikiria kuendelea ku-save hizi hela na kuzielekeza kuliko kurudisha wananchi kufanya chaguzi tena kwa sababu watu wameamua kununua watu na warudi upande wa pili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata chaguzi za marudio zilipofanyika, tumeshuhudia ukiukwaji mkubwa wa taratibu nzima za uchaguzi. Uchaguzi huu tulipofanya tumeshuhudia ilikuwa ni uchaguzi kati ya chama kilichosimamisha mgombea; mfano mimi nilienda Siha, nilienda uchaguzi mdogo wa marudio Jimbo la Arumeru Magharibi, tumeona ni uchaguzi kati ya CHADEMA na Jeshi la Polisi. Nilishuhudia Wakala anatekwa Kituoni, Polisi yupo, hakemei, hasemi kitu; hakuna anayezungumza, maana yake tumeingia kwenye uchaguzi kati ya Vyama vya Upinzani na Jeshi la Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu inaonekana mmeongeza adui mwingine ambaye hamtaki kumsikia wala hamtaki kuona Vyama vya Siasa hasa vya upinzani vikifanya kazi yao, ushauri wangu Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa Serikali yako, ni kuleta marekebisho ya Katiba hapa Bungeni tufute Vyama Vingi ulimwengu ujue, dunia ijue kwamba Serikali ya Awamu ya Tano haitaki kabisa Mfumo wa Vyama Vingi, turudi kwenye mfumo wa chama kimoja. Nadhani hiyo ndiyo itakuwa njia sahihi na mtaendelea kufanya mnayoyafanya kwa kadri ambavyo mtataka.

T A A R I F A . . .

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba tu kumwambia Mheshimiwa Mwigulu kwa sababu unaingia kwenye Cabinet, naomba upokee ushauri wangu kumwambia Mheshimiwa Rais Magufuli, tufute Vyama vya Upinzani nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, waasisi wa nchi hii walituachia tunu za Taifa zikijikita katika umoja, amani na haki, lakini leo tunashuhudia katika nchi hii hakuna umoja. Umoja ule ambao umejengwa na hawa viongozi ambao walitutoa nchi kwenye utumwa na kwenye ukoloni wakatufikisha hapa tulipo, umoja ule haupo. Kwa nini haupo? Kwa sababu tunashuhudia matamko mbalimbali ya viongozi wakiligawa Taifa. Wakiona wananchi hawa wamevamia ardhi, wanasema hawa msiwabomolee kwa sababu walinipa kura; lakini wengine wanabomolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwalimu Nyerere alituachia tunu ya umoja, lakini leo tunu hii inavunjwa, tuliachiwa amani na mmeendelea kuimba kwamba amani ipo, hakuna amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wana hofu. Leo tunashuhudia wananchi wanaopotea, wapo wanaouawa na wako wanaotekwa. Amani ambayo ni tunu ya nchi hii, haipo tena. Kumekuwa na vitisho vingi. Naona leo tunalijenga Taifa kwenye hofu. Watanzania wana hofu. Tunu ambayo tumeachiwa na Waasisi wetu leo inavunjwa na viongozi na Serikali iliyoko madarakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeachiwa tunu ya haki. Haki hii inatiliwa msisitizo kwenye Katiba ambayo ni sheria mama. Katiba inatoa msisitizo wa haki ya Mtanzania kuongea kuonesha hisia zake ama kwa kuandamana ama kwa kuandika kwenye mitandao au kwa kusema chochote ilimradi asivunje sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo watu wanatishiwa, wanakamatwa, wanakuwa na hofu ambazo zimejengwa na watu walioko madarakani, wanachukuliwa hatua kinyume na taratibu, hakuna utawala wa sheria, hatuheshimu wala hatulindi tunu tulizoachiwa na Waasisi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wa malipo wa maji wa pre-paid ukisimamiwa vizuri utaleta tija kubwa na uendelevu wa Mamlaka na Bodi mbalimbali za Maji hapa nchini. Wilaya ya Karatu ni miongoni mwa Wilaya za kwanza kuwa na mfumo huu na mafanikio yameonekana. Je, ni kwa nini Serikali isihakikishe Mamlaka za Maji kwenye miji mikubwa zinaanzisha mifumo hii ambayo itasaidia kufanya mamlaka hizi kuwa endelevu? Nawasilisha.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu kuhusu Mpango wa Maendeleo ya Taifa na nashukuru kwa kuwa mchangiaji wa kwanza jioni hii. Dhima ya Mpango wetu wa Maendeleo ya Taifa wa miaka mitano ni kuangalia suala zima la uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi huu wa viwanda utaendana na ukuaji wa uchumi lakini na maendeleo ya watu. Tunajadili Mpango huo mwisho wa miaka mitano, ni mwaka wa mwisho wa utekelezaji wa Mpango wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilidhani ingekuwa ni vema sana Serikali ikajitathmini katika miaka minne ya utekelezaji wa Mpango; je, tumetekeleza kwa kiwango kipi, tumekwama wapi na tunafikiri nini turekebishe ili yale malengo tuliyojiwekea kwa miaka mitano sasa tuuweke kwenye Mpango huu ambao umebaki wa mwaka mmoja ili kufidia kuziba mapungufu yaliyojitokeza katika Mpango uliopita. Nilidhani wangefanya hivi ingeweza kusaidia sana kujipima kwamba, katika miaka mitano mipango yetu ya miaka mitano ni kiwango gani tupo na tunaendelea vipi, hali yetu ya uchumi ikoje, maendeleo ya watu wetu kwa ujumla yakoje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ni dai la muda mrefu hasa Kambi ya Upinzani, tumekuwa tukidai sana kuwepo na sheria ya kusimamia utekelezaji wa Mpango wa Taifa. Tumedai muda mrefu na hii sheria itasaidi mfano tukifanya tathmini tukaona kuna upungufu fulani na upungufu kama unahitajika kuzibwa na sheria, basi ni muhimu sasa tukawa na sheria ya utekelezaji wa Mpango huu. Tukiwa na sheria hii maana yake pia tutakuwa na uwajibikaji wa kutosha kwa watekelezaji wa Mpango huu lakini tutasaidia kufanya reallocation mbalimbali za bajeti ambazo ziko nje ya mpango. Maana yake mpango ule ambao utakuwa umepitishwa Bungeni kama tutakuwa tuna sheria kwa kiwango kikubwa itaziba hii mianya mingine ya kuibua miradi mingine au mipango mingine mingi mingi ambayo kwa kweli kwa kiasi kikubwa inaenda kuathiri bajeti ambayo tumejiwekea au bajeti ambayo imepitishwa hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kama nilivyosema tukiwa na sheria kutakuwa na uwajibikaji wa kutosha, Serikali itawajibika kwa kuhakikisha kwa kweli mipango inatekelezwa kwa kiwango kikubwa na kwa asilimia hata mia moja ikiwezekana inaweza kufikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kutokutekelezwa kwa miradi ya maendeleo. Tumeona, tunashindwa kutekeleza baadhi ya miradi ya maendeleo kwa sababu tunakuwa na mipango mingi ambayo haiendani na bajeti, haiendani na makusanyo yetu ya ndani, lakini tunakuwa na mipango mingi na miradi mingine mikubwa ambayo kwa kweli kwa kiwango kikubwa hatutaweza kutokana na fedha zetu kutekeleza. Ndiyo maana nikatoa rai hapa mwanzo kwamba ni lazima tufanye kwanza tathmini tuone tumejikwaa wapi, tumeshindwa nini ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona pia Bunge limekuwa likiidhinisha bajeti hapa lakini utekelezaji wa bajeti hiyo hasa kwenye miradi ya maendeleo kwa kweli ni kiwango cha chini sana. Ukirejea hotuba ya Kambi yetu ya Upinzani inaeleza mfano, kwenye Wizara ya Kilimo na Sekta nzima ya kilimo. Tukielewa umuhimu wa Sekta ya Kilimo hapa nchini tunajua ndiyo watanzania wengi wanategemea kilimo lakini kilimo hiki ndiyo tunategemea. Kama tunataka viwanda maana yake tunategemea kilimo tupate malighafi, viwanda viweze kuendelea na hatimaye hicho tunachokisema kwamba tunataka uchumi wa viwanda ili kuchochea maendeleo ya watu na hali ya uchumi kwa ujumla tuweze kufikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutakuwa hatutekelezi miradi ya maendeleo, kama tutakuwa Bunge lako linaidhinisha bajeti hapa halafu hazifiki kwenye wizara husika maana yake tutakuwa hatupigi hatua tunarudi nyuma. Kwa hiyo, ni muhimu sana sana tukaangalia kuwa na miradi michache ambayo tunajua tunaweza kutekeleza na miradi hiyo ikapitishiwa fedha hapa Bungeni na kwa kweli ikatoka kwa asilimia mia moja. Kwa hiyo, ukienda kwenye Wizara ya Kilimo, ukienda kwenye Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ukienda kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara, wizara zote ambazo zinafungamana na hicho ambacho tunakitaka, uchumi wa viwanda zote fedha zake za miradi ya maendeleo kwa kweli hazijafika hata asilimia 60, 70 au asilimia 100. Kwa hiyo, ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, Serikali sasa hivi inatekeleza miradi mikubwa mitatu, kuna Stiegler’s Gorge, kuna SGR na ununuzi wa ndege, hii yote ni miradi mikubwa ambayo inahitaji fedha nyingi. Sasa tunakuwa na miradi mikubwa kwa mara moja ambayo inahitaji fedha nyingi maana yake ni kwamba fedha zozote zinazopatikana zinaenda kwenye miradi mikubwa. Halafu huku kwingine kwenye miradi midogo midogo ambayo kwa kiwango kikubwa ina mgusa mwananchi wa kawaida haifikiwi na hatuwafikii watu wa kawaida. Kwa hiyo, rai yangu kwa Serikali kwamba mnapokuwa na miradi mikubwa mje na mkakati wa ziada wa kuonesha ni namna gani miradi mikubwa inaweza ikatekelezwa, ni namna gani itakuwa financed ili miradi hii iweze kutekelezwa. Ni muhimu sana ili tusiweze kuathiri mambo mengine, utekelezaji wa miradi mingine ya maendeleo kwenye sekta mbalimbali ndani ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukirudi kwenye Serikali zetu za Mitaa kuna hali mbaya sana. Tuligemea kwamba, na tunategemea kwamba Serikali za Mitaa ndiyo kwa kiwango kikubwa ndiyo wananchi wako kule, ndiyo kwa kiwango kikubwa tunategemea miradi muhimu ambayo inamgusa mwananchi mmoja mmoja; maji, barabara, kilimo, masoko, kwa kiwango kikubwa mwananchi kule kwenye Serikali za Mitaa ndiyo inamgusa. Serikali za Mitaa hizi sasa hivi zimekuwa hoi bin taabani, hakuna kitu, fedha zote za makusanyo zimebebwa. (Makofi)

T A A R I F A

MWENYEKITI: Mheshimiwa Keissy taarifa nimekuona.

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba anasema Serikali yetu haipeleki miradi katika wilaya. Tangu uhuru haijajengwa hospitali za wilaya 67, tumejenga zahanati hazina hesabu, sasa nashangaa anasema hatupeleki wakati miaka yote 45 sijui hakuna… kama Namanyere tulikuwa hatuna hospitali ya wilaya acha kwake. Juzi ametoa hospitali ya wilaya pale Ubungo tena kwa mpinzani, sasa anasema wapi hatupeleki miradi midogo midogo!

MWENYEKITI: Amesahau kidogo unajua tena hayo mambo, Mheshimiwa Cecilia si unajua alikuwa kwenye utaratibu maalum! Mheshimiwa Cecilia. (Kicheko)

Tunatumaini mjukuu hajambo! Endelea Mheshimiwa Cecilia. (Kicheko)

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante taarifa ya Mheshimiwa Keissy siipokei na siipokei kwanini! Ukifanya tathmini kwa sababu si toka tumepata uhuru nchi hii inaongozwa na Chama cha Mapinduzi, nchi hii ndiyo inakusanya kodi. Ukifanya tathmini toka tumepata uhuru mpaka leo yaani tulipaswa Tanzania hii kuwa ulaya, kama kwingine maana yake ni tumechelewa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo unapoongelea Namanyere ndiyo wamepata hospitali ya wilaya wamechelewa sana, walipaswa wapate kwenye miaka labda ya 80 huko, 70, miaka ya 90 mnaongelea habari za hospitali za rufaa kwenye maeneo yenu sasa namna gani ya kuboresha. Kwa hiyo, kwa mtazamo wa kwamba ipo inafanyika, imechelewa kufanyika, ilipaswa ifanyike mapema iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niendelee kwenye Serikali zetu za Mitaa nadhani ni rai sasa kwa Serikali kuzitazama upya Serikali zetu za Mitaa, vile vyanzo vingi ambavyo mmevinyang’anya mvirudishie ili viweze kujiendesha. Namna gani itaendesha, namna gani itatumikia wananchi, leo kuna baadhi ya halmashauri hata Vikao vya Baraza la Madiwani kwa mujibu wa sheria havifanyiki kwa sababu hakuna fedha, havifanyiki kwa sababu mapato ni madogo, yale yanayopatikana kidogo yanachuliwa. Siyo tu kuchukuliwa wakati mwingine maagizo yanayokuja kwa kiwango kikubwa kinaenda kufanya nini, kuharibu bajeti ambayo imewekwa kwenye Serikali za Mitaa. Kwa hiyo, bado Serikali zetu za mitaa zina hali mbaya zinapaswa kwa kweli kwa kiwango kikubwa kubebwa na kusaidiwa na kurudishiwa fedha zile ambazo zitakusanywa na Serikali Kuu, zinazotakiwa kurudi kwa mujibu wa sheria zikarudi zikatekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ya kwangu yalikuwa ni hayo machache, nashukuru sana kwa nafasi ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro ya wakulima na wafugaji imekuwa ni migogoro ya muda mrefu hapa nchini. Serikali haijaonesha mikakati ya dhati ya kumaliza migogoro hii. Mara nyingi Wabunge wameitaka Serikali imalize migogoro hii iliyodumu kwa muda mrefu, kuwepo na mipango sahihi ya ardhi, hakika kutapunguza migogoro hii. Naishauri Serikali kwa kushirikiana na Wizara mbalimbali pamoja na Halmashauri za Wilaya ziweke bajeti inayotosheleza na inayotekelezeka ili zoezi la upangaji wa matumizi bora ya ardhi liweze kufanyika au kutekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pembejeo za kilimo na mbolea; kumekuwa na tatizo la ucheleweshaji wa mbolea kwa wakulima hasa msimu unapoanza. Ucheleweshaji ni jambo moja ila hata mbolea halisi inayohitajika na wakulima kulingana na ardhi zao ni tatizo lingine. Tatizo hili ni kubwa sana na linaleta athari kubwa kwa wakulima.
Kwa kuwa Viwanda vya Mbolea ni vichache na kwa kuwa kilimo ni jambo endelevu na hitaji katika maisha ya kila siku ya wananchi wetu, nashauri Serikali iwe na mpango wa muda mrefu wa kuwa na viwanda vya mbolea ambavyo vitaendeshwa na Serikali ili kuondoa na kupunguza kabisa urasimu na upatikanaji wa mbolea hapa nchini.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. KANALI (MST) MASOUD ALI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kuwasilisha hotuba yake nzuri inayoonesha mwelekeo mzuri wa kuletea maendeleo Taifa letu. Pia nimpe changamoto kwamba ajitahidi kwa sababu Wizara hii ndiyo Wizara ambayo iko kwenye kioo cha kila mtu. Kwa hiyo, akifanya kweli ataonekana na asipofanya ataonekana hata kabla ya kuja hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kuchangia kuhusu hali ya anga la Tanzania. Kwa uono wangu kimataifa tunajulikana Tanzania tuna anga la Tanzania, hakuna anga la Zanzibar wala anga la Tanzania Bara. Hivyo basi, ni muhimu tunavyotoa huduma za anga tuzijenge kulenga kufanikisha kwa sifa ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi kirefu sasa kumekuwa na mawasiliano ya muda mrefu kati ya TCAA na Mamlaka ya Kiwanja cha Ndege cha Zanzibar. Kiwanja hiki kwa muda mrefu hakijafungwa kifaa cha Instrument Landing System (ILS) ambacho kilikuwa kifungwe kipindi cha miaka minne, mitano iliyopita, kila siku ahadi inakuwa kitakufungwa. Kweli huduma za ndege zinaendelea lakini hiki ni kifaa muhimu kinachowasaidia marubani kutua wakati wa usiku, mawingu na mvua kwa uhakika na usalama zaidi.
Niombe basi Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie kama hili jukumu si la TCAA, ni bora watoe kauli dhahiri inayosema kwamba hiki kifaa hawatakifunga na hakiwahusu ili sasa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iweze kuchukua jukumu la kutafuta hicho kifaa na kukifunga kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, si vizuri vitu kama hivi vikawa vinatupwa kama mpira. Ni bora kuambizana ukweli ili kila mtu afahamu jukumu lake, lakini litekelezwe ili kuleta ufanisi wa kazi tunazozifanya za kila siku. Tukipata sifa ya anga, nasema mara ya pili, ni sifa ya Tanzania na likitokea tatizo bado mamlaka hizi zitahusika na kutakiwa kujibu maswali ambayo kwa kweli nahisi hayatakuwa muhimu na ya msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nichangie hilo lakini nimkumbushe Mheshimiwa Waziri akisaidie kiwanja hiki cha ndege cha Zanzibar. Nakumbuka lilitolewa jibu lakini nimsisitize tu awasaidie kulipwa lile deni lao la shilingi milioni 230 na ATC. Tunasikia au tumeambiwa madeni yatahamishiwa Hazina, lakini nimuombe tu alipe uzito ili kuwasaidia wenzetu hawa kufanya kazi zao kwa ufanisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliomba dakika tano na nahisi zimenitosha kwa kuchangia jambo hili muhimu sana. Na mimi naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri mbalimbali hapa nchini kuna mabonde yenye mchanga ambapo siku za awali (nyuma) umiliki huo ulikuwa chini ya vijiji husika na kuwezesha vijiji hivyo kupata mapato.
Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni, Wizara ya Nishati na Madini imebadili utaratibu huo na kukabidhi mabonde hayo kwa mawakala mbalimbali ambao wamekuwa wakitoza tozo tofauti kwa kila eneo na wakati mwingine mawakala hawa hutoza tozo hizi katika barabara kuu kwa kuweka road blocks kwa kushirikiana na askari wa barabarani. Kwa kuwa utaratibu wa tozo hizo ni chanzo cha mapato ya Halmashauri za Vijiji na wameweka katika by laws zao; na kwa kuwa utaratibu huo mpya haujawashirikisha vijiji husika, je, Serikali haioni upo umuhimu wa kupitia upya utaratibu huu kwa manufaa ya Serikali za Vijiji hapa nchini?
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Karatu ni mji wa utalii kwa kuwa ni lango kuu la kuingilia Hifadhi ya Mamlaka ya Ngorongoro. Tukitambua mchango mkubwa wa sekta ya utalii katika nchi yetu lakini baadhi ya vijiji katika Wilaya ya Karatu havina umeme. Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Vijiji vya Buger, Gongali, Endamanghang, Kansay na baadhi ya vijiji katika Mji wa Karatu?
Mheshimiwa Naibu Spika, nawasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hoja iliyowasilishwa na Waziri Mkuu hapa Bungeni. Na mimi nitaanza mchango wangu kwa kujielekeza katika ugonjwa huu wa Corona.

Mheshimiwa Spika, watu wamekuwa na mitizamo kwamba ugonjwa huu siyo wa kutisha sana ukilinganisha na ugonjwa mwingine kama UKIMWI, kansa na magonjwa mengine. Hata hivyo, ni ukweli kwamba ugonjwa huu wa Corona unatisha sana kuliko magonjwa mengine kwa sababu ya njia ya uambukizaji wa ugonjwa wenyewe na unatishia uhai wa binadamu na umesababisha vifo vingi katika mataifa mbalimbali ulimwenguni tena kwa muda mfupi sana.

Mheshimiwa Spika, bado hatujaona jitihada za dhati za Serikali za kuhakikisha ugonjwa huu unadhibitiwa. Tumeambiwa na wataalamu na tumeona kwamba tunawe mikono, kwa kweli tunajitahidi kunawa mikono hata Watanzania wananawa sana mikono popote walipo. Tumeona shule na vyuo vimefungwa na mambo mbalimbali ikiwemo makongamano, semina, michezo mbalimbali vyote zimeahirishwa ili wasipate maambukizi haya ya Corona.

Mheshimiwa Spika, hiyo ni hatua moja lakini bado hatujaona hatua nyingine katika maeneo yenye misongamano mikubwa mfano stand za mabasi, mabasi yanayotoka mikoani yanaingia kwenye miji mikubwa, kwenye mabasi kuna misongamano na tumeambiwa ugonjwa huu unaambukizwa kwa njia ya hewa. Sokoni tunakoenda bado kuna misongamano mikubwa sana. Kwenye magereza yetu kuna misongamano, magereza yetu yamejaa kupitiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukumbuke pia tuna cell zetu polisi ambazo wahaalifu kila siku wanaingizwa. Cell za polisi kwa utamaduni uliopo zinajaza wahalifu kupitiliza na hawapimwi. Mfano muhalifu akipatikana leo wala yeye hatawekwa kwenye chumba kingine cha karantini kwa siku 14 halafu achanganywe na wahalifu wengine kwa sababu hatuna hata hivyo vyumba vya kuwahifadhi katika vituo vyetu vya polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,ndiyo maana nikasema hatua za awali zilizochukuliwa kukabiliana na ugonjwa huu bado hazitoshi, tunahitaji jitihada kubwa sana za kukabiliana na ugonjwa huu kwa sababu ya namna ambavyo unaambukizwa na jinsi ambavyo tumeona katika nchi za Ulaya, Marekani na China watu walivyokufa. Siyo huko tu, tujiangalie hata katika block ya Afrika Mashariki jinsi ambavyo ugonjwa huu umeweza kuuwa watu wengi.

Mheshimiwa Spika, kwa nini bado nasema Serikali inahitaji kujipanga sana kwenye ugonjwa huu wa Corona? Tuna maabara moja tu ambayo ndiyo inapima na kutoa majawabu ya watu walioathirika na virusi hivi vya Corona. Maabara hii ipo Dar es Salaam tu, hata hapa Makao Makuu ya nchi haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunajiuliza, kama mfano ikitokea kuna mgonjwa katika Wilaya ya Tanganyika labda kule Katavi au Kigoma mpaka sampuli iletwe Dar es Salaam itolewe majawabu, kama mtu huyu hajawekwa karantini huko aliko, kwa kweli tutakuwa tunajiweka kwenye wakati mgumu kama nchi. Serikali iliyopo madarakani nyie mmejipambanua kama ni Serikali wanyonge lakini tutawaonaje mkiwatetea wanyonge hawa wa Tanzania katika janga hili kubwa la Corona ambalo linauwa watu kwa upana mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, lakini bado tunahitaji kupata majibu na Serikali ituambie. Binafsi nilitegemea tulipoanza Bunge hili Serikali ingetuletea mkakati wa kina na wa dhati wa namna gani wanaenda kupambana na ugonjwa huu wa Corona. Tunajiuliza kama nchi hivi ongezeko likiwa kubwa, mpaka jana tumeona wagonjwa wamefika 20, tulikuwa na wagonjwa 13 leo wamefika 20. Tunajiuliza kama idadi hii ya maambukizi itaendelea kuongezeka, hivi tuna vitanda vya kutosha vya kulaza wagonjwa hawa? Tuna madawa ya kutosha kusaidia kama ambavyo wanafanya kwenye nchi nyingine, tunajua dawa haijapatikana lakini angalau kutibu katika zile hatua za awali? Je, tuna mashine za kutosha za kusaidia kupumua kwa wagonjwa hao? Kwa sababu tumeambiwa ugonjwa huu unashambulia mfumo wa upumuaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunajiuliza hivi tuna madaktari na manesi wa kutosha wa kuhudumia kama janga hili likiongezeka? Leo tuna upungufu wa asilimia 52 ya watumishi wa afya hapa nchini. Je, idadi hii ikiongezeka, hatuombi iongezeke kila mtu hapa anatishika kwa sababu ugonjwa huu ukija haijali wewe ni CCM, CHADEMA, CUF, Muislam au Mkristo, yeyote yule unaweza kumpata. Ugonjwa huu hauchagui mtu lakini tunajiuliza ni kwa namna gani Serikali mmejipanga tuone jambo hili linadhibitiwa kama ambavyo nchi zingine wameweza kudhibiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa zaidi na sijui kama Serikali mnakiri kwamba ugonjwa huu ukiendelea hapa nchini ni kwa hakika uchumi unakwenda kuanguka. Hili siyo la kubisha, uchumi wa nchi na wa mtu moja moja unaenda kuporomoka.

Mheshimiwa Spika,nitoe mfano, sekta ya utalii, mimi natoka Wilaya ya Karatu, tuna hoteli za kitalii 58, leo hoteli zinafungwa, wafanyakazi wanarudi majumbani, wengine wanarudishwa hakuna kazi tena mpaka pale ambapo hali itatengamaa. Hoteli hizo zinategemea watalii wengi kuja na watalii wetu wengi wanatoka nchi za nje na hawaji kwa sababu huko kwao tayari hali ni mbaya. Je, hapa hatujagusa uchumi wa mtu mmoja mmoja na uchumi wa taifa?

Mheshimiwa Spika,lakini leo tunapoanza tu kujadili bajeti ya nchi kwenye sekta ya utalii tu Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro katika mwaka 2018/2019 inaingiza shilingi bilioni 143, kwa hali hii ya Corona hizi fedha tunaenda kuzipata? Hatuwezi kuzipata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, je, hapa hatujagusa uchumi wa mmoja mmoja na uchumi wa taifa? Leo tunapoanza hata kujadili bajeti ya nchi, kwenye Sekta ya Utalii tu, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro katika mwaka 2018/2019 inaingiza shilingi bilioni 143. Kwa hali hii ya Corona hizi fedha tunaenda kuzipata? hatuwezi kuzipata.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kupitia Waziri wa Fedha, lazima atuletee mpango wa haraka hapa Bungeni wa namna gani ya kukabiliana na suala la uchumi wa nchi na uchumi wa mtu mmoja mmoja hasa kutokana na janga hili la Corona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusijifunze tu, tuangalie katika nchi za karibu tu hapa, kwa sababu kuna watu wanaosema kwamba tusitazame nchi zilizoendelea; Italy, Marekani na kadhalika. Hapana, hebu tutazame wenzetu wa jirani; Kenya na Uganda kwa hatua ambazo tayari wameshazichukua. Mfano tu mmoja, leo benki za Kenya zimetoa unafuu wa mikopo kwa siku karibia 90 kwa watu wao. Serikali ya Kenya imewataka wenye nyumba wawape nafuu wapangaji wasilipe kodi kwa kipindi fulani. Hii ni kwenda kumsaidia mtu mmoja mmoja kutokana na hali iliyoko. Sasa sisi kama Serikali ya hapa, watuambie wamejipangaje na jambo hili? Hili jambo halihitaji mzaha wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine hapo hapo kwenye kuwasaidia wapangaji, tunashangaa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam; kwanza mnakataza msongamano, yeye anaenda Mwenge, anaenda Ubungo, anakusanya watu, anaongea, anasema sijui naye anaanza kuongea na wenye nyumba wasamehe wapangaji. Hivi kweli tuko serious? Tumesema tufute misongamano yote kila mahali, kiongozi unaenda unakusanya watu.

Mheshimiwa Spika, halafu tunajiuliza, yeye Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salam ndio amekuwa msemaji wa nchi hii? Suala la kuangalia namna gani wenye nyumba wanatoa unafuu kwa wapangaji, mimi nadhani lichukuliwe na Serikali lifanyiwe na…

SPIKA: Mheshimiwa Cecilia, nilidhani sisi Wabunge tungekuja na mapendekezo kwa Serikali badala ya kuitegemea Serikali peke yake ndiyo ifikirie halafu ije na mpango fulani. Pamoja na Serikali kutakiwa ikifirie, ije na mpango, lakini nasi tuwe tunapendekeza.

Nilikuwa nawaza tu, hili la kusema kwamba Serikali itoe amri, mwenye kajumba kake basi apangishe bure, sijui kama una nyumba yako halafu ipangishwe bure kwa sababu Serikali imesema, sijui kama… hebu weka sawa kidogo hili, maana yake, nilikuwa namwona Mheshimiwa Lema, maana yeye ni tajiri wa nyumba nyingi, sasa anasita hapo. Itakuaje hapo?

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nadhani hujanisikia vizuri, sijasema hivyo na nimeshauri kwamba Serikali ijifunze kwa majirani zetu katika bloc ya Afrika Mashariki jinsi wanavyofanya na tuangalie na sisi hali ya kwetu ikoje. Ndiyo maana nikashauri kwamba Waziri wa Fedha naye atuletee mpango wake kwa jinsi gani tunaenda kuangalia uchumi wa nchi utakavyoporomoka na hatua gani zitachukuliwa kwa uchumi wa nchi na kwa uchumi wa mtu mmoja mmoja. Ndicho nilichosema. (Makofi)

SPIKA: Ndiyo ukatoa mfano kwamba Kenya imesema nyumba sijui imefanyaje.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, naomba niendelee. (Kicheko)

SPIKA: Si unaona lilivyo gumu. Haya endelea Mheshimiwa Cecilia. (Kicheko)

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, kingine ambacho Serikali inapaswa kukifanyia kazi na kuchukua ushauri huu, kama tatizo litaendelea, ni kwa kiasi gani kama nchi tuna hifadhi ya chakula? Huo nao utakuwa ni mtihani mkubwa sana kwa sababu tunaelewa hali ya watu wetu. Watu wetu ni wa kwenda asubuhi…

SPIKA: Mwaka huu chakula kingi sana. Hata kabla Serikali haijasema, kingi kweli kweli! Hata Dodoma hatuombi chakula mwaka huu.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama unasema kingi, basi Serikali ituletee taarifa hapa Bungeni kwamba ni namna gani inaweza kukabiliana na hali ya upungufu wa chakula kama hali ya maambukizi ya ugonjwa wa Corona itaendelea na ugonjwa wagonjwa wataendelea wengi? Sasa hilo litakuwa la msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesema hayo kwa sababu tunaelewa watu wetu ni wa kwenda sokoni leo akanunue kitu kidogo apate riziki, siku iende kesho hivyo hivyo. Sasa kama ikifikia hatua wagonjwa wataongezeka, maana yake lazima tutaenda lockdown. Kama tutaenda kwenye lockdown, namna gani watu hawa tunahakikisha kunakuwa na chakula cha kutosha?

Mheshimiwa Spika, Serikali yoyote duniani panapotokea majanga na milipuko, jamani kitu cha kwanza ni mwananchi. Uhai na afya ya mwananchi, mengine ndiyo yanafuata. (Makofi)

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ushauri wangu kwa Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Naambiwa tayari. Malizia hiyo sentensi yako ya mwisho.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali, bado Watanzania wanahitaji majibu na mikakati ya dhati, Serikali iwaambie Watanzania kwamba namna gani inaenda kukabiliana na ugonjwa huu wa Corona?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Mpango huu wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano. Nitajikita katika mambo machache kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, ni kwenye suala la afya. Ni ukweli usiopingika kwamba, kama wananchi wetu wakiwa na afya imara na Madhubuti, bila shaka Taifa hilo litakuwa ni lenye neema, ni Taifa ambalo litastawi kwa vizazi na vizazi.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu inapaswa ijikite katika afya za msingi, kwa maana ya kwenye Zahanati zetu. Tukiboresha afya inayotolewa, matibabu yanayotolewa katika Zahanati zetu, kwa hakika huu msongamano ambao tunaukuta kwenye Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya, Hospitali za Rufaa kwa kiwango kikubwa tutapunguza.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikijisifia hapa kwamba imejenga vituo vya afya vingi na kadhalika na imeeleza mambo mengi, imejenga vituo vya afya vingapi. Sawa, mmejenga, lakini vipi kuboresha huduma zinazotolewa katika zahanati zetu? Tukiweka mkakati wa kuhakikisha zahanati zetu zina maabara ya kutosha yenye vifaa vyote vinavyotakiwa, watumishi wa afya wanakuwepo kwenye level kabisa ya chini ya zahanati. Pia kuhakikisha miundombinu yote kwa maana ya nyumba za Madaktari, Manesi, barabara inayoelekea kwenye hivyo vituo, kuhakikisha vinapitika mwaka mzima, maana yake tutakuwa tumemsaidia mwananchi yule wa chini kabisa ambaye anakaa karibu kabisa na zahanati.

Mheshimiwa Spika, tukumbuke kwamba, mwananchi wa kawaida akiugua huduma yake ya kwanza ni kwenye zahanati kwa sababu pia iko karibu na yeye, anaweza kuifikia, tofauti na hata akitaka kutafuta huduma hiyo kwenye ngazi ya kituo cha afya. Kwa hiyo ni vema sana Serikali ikaona umuhimu wa kuwekeza na kuweka nguvu kubwa kwenye huduma ya afya katika ngazi ya msingi ambayo inamgusa mwananchi moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna mada hapa asubuhi, mjadala mkubwa kuhusu ununuzi wa ndege na Shirika letu la Ndege. Mpango sasa hivi unaonesha kuna kununua ndege zingine nne, wanaweza kufikiria kuacha kununua hizo ndege, zilizopo tuziboreshe, hiyo fedha tukapeleka kwenye zahanati zetu kuziboresha moja kwa moja tutakuwa tumemgusa Mtanzania wa chini kabisa kwa sababu sio Watanzania wote ambao kwa namna moja ama nyingine wanaweza kuwa na mwingiliano au kufaidika moja kwa moja na ndege tutakazonunua, lakini ukiboresha zahanati kwa namna yoyote ile umemgusa yule mwananchi wa chini kabisa, yule mpigakura wetu, yule mwenye uhitaji wa kutosha wa kuhakikisha anapata huduma bora katika zahanati zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipengele kingine katika Sekta ya Afya, ningependa kuchangia pia kuhusiana na suala la magonjwa yasiyoambukiza. Asilimia 33 ya vifo vinavyotokea hapa nchini vinatokana na magonjwa yasiyoambukiza. Magonjwa yasiyoambukiza wataalam wanasema yanatokana na lifestyle, namna tunavyoishi, ukiacha mengine ya kurithi na kadhalika, lakini mengi ni namna gani tunavyoishi, pressure, sukari, moyo, saratani, figo na kadhalika na ndivyo nilivyosema kwamba asilimia 33 ya vifo vinatokana na magonjwa ya namna hii.

Mheshimiwa Spika, haya magonjwa yasiyoambukiza, kama Serikali ikaweka mkakati wa dhati wa kuhakikisha tunawekeza kupunguza magonjwa haya yasiyoambukiza kwa kushirikiana na jamii na wadau wengine bila shaka tutapunguza vifo hivi, hata mwisho wa siku ule msongamano wa wananchi wetu kukimbilia huduma zote ambazo zinatakiwa kwenye zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya za kanda na za rufaa utapungua, kwa sababu tutakuwa tumejikita katika kuona namna gani tunapunguza magonjwa haya yasiyoambukiza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi leo wote ambao tumesoma bila shaka tulikuwa tunafahamu, leo mtoto yeyote au hata sisi tuliosoma enzi hizo tunafahamu kabisa tunaambiwa, unapata malaria kwa sababu utang’atwa na mbu, ipo ni masomo yanafundishwa, ni mtaala upo na unafundishwa na watoto wanakua wakijua kabisa niking’atwa na mbu nitapata malaria. Sasa vivyo hivyo Serikali inatakiwa kufikiria kuingiza mtaala wa namna gani mtoto huyu anakuwa akifahamu kwamba kuna magonjwa yasiyoambukiza na naweza kukabiliana nayo kwa elimu nitakayoipata. Kwa hiyo ni vyema sana Serikali ikafikiria katika mpango wake namna gani ku-appear kupitia mitaala yetu kuingiza jambo hilo na lenyewe likawa sehemu kama ambavyo tunafundishwa kuhusu malaria na mambo mengine mengi, mwisho wa siku tutakuja kuona, inawezekana tusiyaone matokeo kwa muda mfupi, lakini kwa muda mrefu tukaona matokeo ya kile ambacho tunakieleza. Kwa hiyo ni muhimu sana Serikali ikaweka mpango thabiti wa kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Spika, pia kutoa elimu kwa jamii ni muhimu sana. Kuna wataalam walikuwa wanatupa takwimu sisi Kamati yetu. Wanasema ni fahari leo kwa sisi wazazi unamchukua mtoto wako unampeleka asubuhi na gari lako kwenda shuleni na anarudishwa nyumbani jioni. Akifika anakaa kwenye kochi, anasema mama nataka chipsi mayai anapewa, anakaa kwenye kochi, labda mzazi ana na tablet kidogo anachezea, anaangalia TV, inafika jioni anakula analala, yaani hiyo inakuwa ni lifestyle, kumbe mtoto huyu anaandaliwa mazingira ambayo mwisho wa siku katika ukuaji wake anaanza kupata magonjwa yasiyoambukiza. Uzito kupita kiasi, sukari mwisho wa siku hata uwezo wa kufikiri na kuchanganua mambo unapungua kwa sababu ya lifestyle.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hapa iko haja ya Serikali kwa kushirikiana na jamii kutoa elimu ya kutosha, yaani tusione kwamba huo ndiyo ukisasa au ndiyo style Fulani, wale wataalam wamekuja wametuambia kwamba walivyofanya utafiti kwenye aina ya wazazi ambao wanahudumia watoto wao kwa namna hiyo na yule ambaye anapanda daladala asubuhi kwenda shuleni, wakakuta kwamba mtoto huyu ambaye mzazi wake anamlea kama mayai ana-risk kubwa sana ukilinganisha na yule ambaye atapambana kivyake kutembea kwenda shule au atapambana kwenye daladala kwenda shuleni, yule automatic atajikuta mwili wake unafanya kazi kuliko hata yule ambaye tunampeleka asubuhi na gari kwenda shuleni na anarudishwa na gari na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niishauri Serikali katika mipango yake hii, lazima iangalie namna bora ya kuigeuza jamii yetu kulingana na maisha tunayoishi leo. Unaona tunafurahi kwenda kwenye ma-supermarket makubwa unaingia labda hapo shoppers, unaenda Mlimani City na kwingineko, tunachukua samaki waliohifadhiwa kwenye makopo, basi tunaonekana kama ndiyo tuna maisha fulani mazuri, kumbe tunajiandalia matatizo. Yaani mtu anayeenda maeneo hayo anaonekana ni bora kuliko yule anayeenda Majengo pale sokoni Dodoma. Kumbe yule ni bora zaidi kwa sababu anapata kitu fresh! Anapata matunda fresh kutoka shambani, anapata labda samaki fresh, nyama ya ng’ombe fresh!

Mheshimiwa Spika, sasa hii ni kuangalia namna gani tunabadilisha mind-set ya jamii tunayoiongoza, Serikali wakaweka kitengo maalum au fungu maalum kwa kushirikiana na wadau, kushirikiana na jamii na viongozi sisi wa kisiasa, tukaendelea kuibadilisha jamii yetu kuishi kwenye lifestyle ambayo itatusaidia ili mwisho wa siku tuepukane na magonjwa yasiyoambukiza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya pili inajikita katika Sekta ya Utalii. Bila shaka Serikali na wadau mbalimbali tumeona kwamba jinsi gani ambavyo corona ilivyofika imeathiri kwa kiwango kikubwa Sekta ya Utalii na imeathiri mpaka yule mtu mmoja mmoja ambaye anategemea utalii ule. Naongea hivyo kwa sababu natoka Mkoa wa Arusha na nafahamu jinsi ambavyo watu katika Sekta ya Utalii wameathirika kwa kiwango kikubwa. Sasa huko nyuma tuliongea na kuishauri Serikali iangalie namna gani ya kuweka mipango, inapotokea dharura za namna hii wafanyabiashara na wale wanaonufaika moja kwa moja na Sekta hii ya Utalii wapunguziwe mambo fulani fulani yanayowaumiza.

Mheshimiwa Spika, mfano, hoteli nyingi zilifungwa wakati wa corona, nyingi mno kukawa hakuna wageni, wakapunguza wafanyakazi lakini mwekezaji au mtu yule mwenye hoteli hajawahi kupunguziwa kodi na Serikali hata siku moja, tena alitakiwa alipe na wengine kodi zikaongezeka. Sasa sina uhakika sana kama tunataka kweli kuendeleza utalii ambao unachangia pato kubwa la Taifa au tunataka kuumaliza na kuukandamiza. Kwa hiyo nishauri kwamba ni vyema panapotokea majanga ya namna hiyo, hatuyaombei lakini yanaweza yakatokea, ni lazima kwenye Sekta ya Utalii pamoja na sekta zingine Serikali iwe na mipango ya kuhakikisha inatoa unafuu au kwa mwekezaji mmojammoja au wawekezaji kwa ujumla ambao moja kwa moja wanaungana, kunakuwa na mnyororo wa moja kwa oja ambao unamgusa mwananchi mpaka chini kuhakikisha inatoa unafuu wa mambo fulani fulani ambayo yatamfanya mtu huyu aweze kuendeleza biashara ile ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado inatakiwa mikakati ya kuendeleza na kukuza utalii wetu. Bado tunahitaji kuwa na mikakati mizuri ya kuhakikisha Serikali inapata mapato katika utalii wa picha, hatujawekea mkazo na huko nyuma ripoti ya CAG zimeeleza mara nyingi kwamba Serikali imekuwa ikipoteza fedha nyingi kwa sababu haiweki mpango thabiti wa kuhakikisha utalii wa picha unatuingizia pato na kuhakikisha unasimamiwa vizuri. Vivyo hivyo kwenye Sekta ya Uwindaji pia inapaswa kuwekwa mipango thabiti ya kuhakikisha kwamba inaingiza kodi ambayo mwisho wa siku itatusaidia.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie kidogo pia kuhusu Serikali zetu za Mitaa hapa nchini. Halmashauri zetu nyingi zimepokonywa mapato, mwisho wa siku zinashindwa kujiendesha, mwisho wa siku ufanisi unaotarajiwa hauwezi kufikiwa kwa sababu hamna mapato yale yanayokusudiwa. Kwa hiyo niishauri Serikali, kuna mapato ambayo Serikali iliyachukua haiwezi hata hiyo TRA yenyewe kukusanya bado imekuwa ni changamoto, niishauri irudishe kwenye Serikali za Mitaa. Ikirudisha kwenye Serikali za Mitaa pawepo na usimamizi thabiti, pawepo uhakika kwamba kile kilichorudishwa kinatumika moja kwa moja na kinafanya kazi ambayo inakusudiwa. Hiyo itatusaidia sana kwa sababu kwenye wananchi ni kwenye Serikali za Mitaa, ndiyo tunamgusa mwananchi moja kwa moja kule chini. Ukiziwezesha na kuzisaidia halmashauri zetu moja kwa moja umemgusa Mtanzania. Kwa hiyo ni vyema sana Serikali ikalitazama jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi, mno! Ripoti ya CAG na taarifa mbalimbali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Cecilia Paresso.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie. Ripoti mbalimbali zinaonesha kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi vivyo hivyo basi ni vyema Serikali ikahakikisha watumishi wanapatikana. Watumishi wa kutosha wakiwepo, ukirudisha mapato, ukasimamia vizuri, matokeo tunayoyatarajia kwa nchi yetu yataweza kufikiwa. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Fedha. Wizara ya Fedha na jukumu la kusimamia uchumi wa nchi, lakini ina sera mahususi kwa mambo mengi kama yalivyoorodheshwa katika instrument yake na mojawapo ikiwa ni kuweka mkakati wa kusimamia utekelezaji wa kupunguza umaskini.

Mheshimiwa Spika, katika suala zima la ukusanyaji wa mapato kwa maana ya zoezi zima la ulipaji wa kodi, naendelea kuishauri Wizara kuweka mazingira mazuri, rafiki, kodi zinazolipika, bila shaka na kwa imani kubwa wafanya biashara wote watalipa kodi kwa amani kabisa, bila kuwepo na kusukumana, kuwekeana kodi kubwa kubwa, kupelekeana task force zinazoumiza wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiamini kupitia makosa yaliyofanyika huko nyuma ya kupeleka task force, kuongezea watu kodi, kulazimisha watu kulipa kodi wakati alishalipa kodi, tuna imani kabisa kupitia Rais mama Samia haya mambo hayatajirudia na wafanyabiashara watafanya biashara zao katika mazingira mazuri na rafiki na watapenda. Kwa sababu, huko nyuma ilikuwa ikifikia kwamba, mfanyabiashara akimwona afisa wa TRA anaenda, ni sawa sawa na amemwona simba mlangoni kwake. Sasa tutoke huko iwe mfanyabiashara akimwona afisa wa TRA, awe anamfurahia na kumkaribisha na kama ni kuhakiki kodi, kama ni masuala ya kodi, yanazungumzika katika namna rafiki na namna ambayo itamwezesha mfanyabiashara awe na amani pale ambapo anafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni sambamba na kusema kwamba, wote tunawajibika kulipa kodi ile ambayo tunapaswa kulipa. Baada ya utangulizi huo, napenda kuiuliza Wizara, hivi wafanyabiashara wa maduka ya kubadilishia fedha waliwakosa kitu gani kwa nchi hii? Niliwahi kuongea katika Ofisi ya Waziri Mkuu jambo hili hili na nataka leo nilirudie kwa sababu ni Wizara husika. Waliwapora wafanyabiashara wa maduka ya kubadilishia fedha katika Mkoa wa Arusha, Mkoa wa Kilimanjaro na Dar es Salaam. Sina hakika kama waliwapa sababu sahihi ya kwa nini walipeleka task force na nguvu kubwa kuwanyang’anya fedha wafanyabiashara hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukisikia kwa pembeni, ni kwamba, walikuwa hawakulipa kodi. Hivi inawezekanaje, pamoja na machinery zote walizonazo mtu anafanya biashara hii kwa miaka kadhaa, halafu inatokea tu kwamba leo hawajalipa kodi. Haya, kuna hisia nyingine kwamba, maduka haya yalikuwa yanatumika kupitishia fedha haramu, sasa kama yalikuwa yanatumika kupitishia fedha haramu, je, ni kweli wafanyabiashara wote wa nchi hii wa maduka ya fedha walikuwa wanatumika kupitisha fedha haramu? Kama sivyo, kwa nini waliwaadhibu wote? Kama ndivyo, maana yake kuna upungufu mahali na kama kuna udhaifu na upungufu mahali, ama ni wa kisera, ni wa kisheria, wamechukua hatua gani kwa hicho kilichosababisha kupelekea hapo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nataka Mheshimiwa Waziri atuambie baada ya kuhitimisha hoja hii, wale wafanyabiashara ambao walikuwa innocent, ambao walikuwa na leseni za biashara, ambao walikuwa wanalipa kodi, ambao wamewanyang’anya fedha zao, nini hatima ya wafanyabiashara hawa ambao walikuwa wanaendesha biashara hii kihalali kabisa? Tunataka kufahamu wafanyabiashara hawa fedha zao ziko wapi na watawarejeshea lini? Halafu, wapo wengine ambao waliwalazimisha mfano, wamechukua labda bilioni moja, mnalazimisha kwamba, alichukua labda milioni 600 unamlazimisha asaini fedha ambayo haikuchukuliwa kihalali. Hii sio sawa, tunataka kupata majibu ya hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama sera ya Serikali inasema ni kupunguza umaskini, hivi wanapunguza umaskini au wanaongeza umaskini! Naona wanaongeza umaskini. Kwa hiyo, hili halikubaliki, lazima wafanye marekebisho na lazima wakutane na hawa watu. Namshauri Mheshimiwa Waziri akutane na hao wafanyabiashara, waongee nao, wasemezane nao, hawa watu wajue hatima ya fedha zao ambazo wamezipata kihalali ni nini ili wajue wanafanya nini.

Mheshimiwa Spika, napenda pia, kufahamu, wame- cease hii biashara ya maduka ya kubadilishia fedha, lakini wanayarejesha. Wanayarejesha kwa masharti magumu sana, wanataka kurejesha kwa kusema mtu ambaye anataka sasa kuendesha maduka ya kubadilishia fedha, awe na mtaji wa bilioni moja, hii inawezekana kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndio maana nasema hii sera waliyojiwekea ya kusema wanataka kupunguza umasikini, hivi wanapunguza ndio wanauongeza? Hizi biashara za kubadilishia fedha yalikuwa ni maduka hasa mipakani kwetu Namanga, Holili, Sirari, Tunduma na maeneo yote ya mipakani, yalikuwa ni maduka ambayo kwa namna moja au nyingine yalikuwa yanatoa ajira pia kwa vijana wetu. Vijana walikuwa wana maduka madogo wanabadilisha fedha twenty-four, seven, leo unamwambia awe na mtaji wa bilioni moja. Sasa nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri, ni busara hii ya kupunguza umaskini au ni busara ya kuongeza umaskini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi wanaweka masharti kwamba, mtaji uwe bilioni moja, halafu uwe na Mkurugenzi, wewe ambaye unataka kuanzisha duka hili la Bureau de Change, uwe na Marketing Manager, uwe na Internal Auditor, haya ni mambo ambayo hayawezekani. Hivi kwa nini, tusiiache hii biashara huria, watu wafanye lakini kuwepo na control measures, ambayo itasimamiwa na BOT, kuhakikisha kama kuna harufu ya fedha haramu, kuwepo na hiyo measures ambayo itadhibiti jambo hili. Sio kwamba, tunawakatisha watu wasifanye biashara hizi, tunataka tu eti benki ndio ifanye na tunajua benki ikifika saa 9.00, saa 10.00 wamefunga. Sasa ikifika saa 9.00, saa 10.00 amefunga, mtu ambaye anataka kwenda kubadilisha fedha anaenda kupata wapi hii huduma? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaongea habari ya kukuza utalii, tunatambua sekta ya utalii, mtalii anashuka Airport na KLM ya saa 6.00 usiku pale Kilimanjaro. Anataka kesho yake kwenda porini, safari, anataka kubadilisha fedha, atasubiri hiyo benki kesho yake ifunguliwe saa 2.00 ndio akabadilishe fedha ndio aweze kuendelea na utaratibu mwingine? Kwa hiyo, nafikiri iko haja ya kulitazama na kuachia biashara hii huru, watu waendelee kufanya hii biashara, lakini kwa kudhibiti ule upungufu uliojitokeza, kwa kuweka mikakati thabiti ambayo inaweza ikamfanya kila mtu akaingia kwenye biashara hii, tukaendelea kukuza ajira, tukaendelea kuhakikisha tunawapatia vijana wetu ajira na mazingira rafiki zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichangie pia, suala la wakandarasi. Wabunge wengi wamechangia kwa hiyo, niongezee kwa kusema kwamba, kwa kweli wakandarasi wanaodai fedha Serikali walipwe. Hawa wakandarasi wengine wameenda kuchukua fedha benki, wanadaiwa na mabenki, wamefilisika leo kwa sababu Serikali haijawalipa kwa wakati. Wanafanya uhakiki, uhakiki gani wa miaka mitano, sita jamani, uhakiki gani ambao hauishi! Haya ni mambo ya kushangaza sana! Ndio maana nikasema, narudi kwenye ile ile sera ya Serikali. Hivi unampa mkandarasi kazi, unataka umnyanyue kiuchumi, hapo hapo unamkandamiza, humlipi, maana yake unampa umaskini, humwongezei faida yoyote, husaidii uchumi wa mmoja mmoja kuweza kukua. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa, Mheshimiwa Esther Matiko.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nataka nimpe taarifa, Mheshimiwa Paresso kwamba sio tu kwamba wanafilisika, bali hata hao wakandarasi unajua wanakuwa wana watu wamewaajiri. Kwa hiyo, inabidi wawapunguze kutoka makazini, lakini wengine kwa sababu, wana majumba na vitu vingine ambavyo wameviweka kama guarantee kule benki wakishachukuliwa wanaamua kujiua. Kwa hiyo, kuna Watanzania wengi sana ambao wamepoteza maisha, kwa sababu ya madeni ambayo yamekaa zaidi ya miaka minne mpaka mitano, Serikali ikisema inahakiki hayo madeni. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Paresso unapokea hiyo taarifa?

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, naipokea hiyo taarifa. Ni kweli kabisa, wakandarasi hao wako wengine wameweka nyumba zao dhamana zinachukuliwa, zinapigwa mnada. Wengine wanakata tamaa hawaoni matarajio na matumaini yoyote ya fedha zake kulipwa anaamua kujiua. Haya mambo yapo, tunayakuta kwenye jamii, tunakutana na hao watu. Ni wakati sasa, Wizara walichukulie jambo hili kwa uzito na kwa umuhimu wa kipekee kuhakikisha kwamba, wakandarasi wote wanalipwa fedha. Wanajua mimi sio Mchumi, lakini impact tu inaonekana, ukiwalipa wakandarasi maana yake pia, unarudisha mzunguko wa fedha kwenye jamii. Tunataka tuone hilo lifanyike na jamii iweze kupata hiyo impact ya wakandarasi hao kulipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema, Wizara ni vyema sasa na wale wafanyabiashara ambao walipelekewa task force, wakaambiwa walipe sijui malimbikizo ya kodi ya miaka sijui mingapi iliyopita, narudia kusema na kuishauri Wizara na Serikali kwa ujumla kwamba, hao wafanyabiashara, tunaomba sana hizo task force zisichukuliwe kama sehemu ya kodi, waachane na hiyo biashara, wapewe comfort ya kufanya biashara. Kama kuna haya madeni wanayodaiwa huko nyuma, nafikiri tunafungua ukurasa mpya wa kuwapa wafanyabiashara mazingira mazuri na rafiki ya kufanya kazi, lakini na wao wakijua wana wajibu wa kulipa kodi kwa ajili ya maendeleo ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali iliyoko mbele yetu. Tukitambua hii ni bajeti ya kwanza ya Serikali ya Mheshimiwa Mama Samia, niseme tu kwamba nampongeza kwa sababu kuna mambo mazuri ambayo yapo kwenye bajeti yanayoleta matumaini na mengine pia nitayashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza jambo zuri ambalo nimeliona hapa na kwa nini nasema nalipongeza? Kuweka bajeti kwa ajili ya kupandisha madaraja watumishi wetu wa Umma. Hili ni jambo zuri kwa sababu watumishi wetu wa Umma ndio injini ya nchi hii. Hawa Watumishi wa Umma walisahaulika muda mrefu, hawakupanda madaraja, hawakuongezewa mishahara. Kwa hatua hii ya awali ya kuweka bajeti kwa ajili ya kupandisha madaraja, tunampogeza sana Mheshimiwa Mama Samia. Tunaomba aendelee hivyo ili huko mbele ya safari aweze kuongeza na mishahara ambayo Watumishi wa Umma muda mrefu hawajapata Nyongeza hii ya mishahara lakini hawajapanda madaraja.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kwa nini nasema nampongeza? Imekuwa ni matamanio ya Madiwani muda mrefu kwa nchi nzima, nami nilikuwa Diwani. Nililvyoingia mara ya kwanza katika Bunge hili ilikuwa pia ni hoja yangu ya kuona namna bora ya kuboresha utendaji kazi wa Madiwani hapa nchini. Mama Samia ameliona tunampongeza kwa kuchukua hatua hii, kwamba sasa Madiwani walipwe na Serikali Kuu badala ya Halmashauri zetu za Wilaya ni hatua nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, twende mbali zaidi sasa, tuwajengee uwezo Madiwani, tuwape semina mbalimbali kwa sababu sasa watakuwa wametoka kwenye vile vifungo vya kuwatumikia Wakurugenzi ili wasikose posho zao, watakuwa independent, wataweza kujisimamia, kusimamia fedha zinazoenda, kusimamia miradi. Basi tujikite pia kuona namna bora ya kuwapa mafunzo ili fedha tunazopeleka katika Local Government kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo isimamiwe vizuri kwa uwezo na tuliowajengea Madiwani wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine muhimu, kuna masharti, kanuni, taratibu mbalimbali ambazo zimeondolewa, ambayo ni hatua nzuri ya kupunguza urasimu wa nchi hii. Nimeona kuna baadhi ya vitu vimeondolewa, siyo lazima vipite kwenye GN, siyo lazima sasa vikae Baraza la Mawaziri, vimempa mamlaka Waziri. Ziko tozo na adhabu na faini na misamaha mingine ambayo pia amepewa Kamishna wa TRA. Ni hatua nzuri ya kwenda kupunguza urasimu ili yale matokeo tunayoyatarajia yaweze kufikiwa. Hongera sana kwa hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba mama alishajipambanua kwa kusema kwamba hataki kodi ambazo ni za dhuluma. Sasa tunaomba haya ambayo ameyatenda mama, watendaji wake na wasaidizi wake mkayafanye kweli kweli. Tunataka wafanyabiashara wetu ili waweze kulipa kodi, wawe na mazingira mazuri, rafiki yanayofikika, ambapo kweli watafanya biashara na watalipa kodi na uchumi wa nchi utakua na uchumi wa mtu mmoja mmoja utakua na kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, haya ambayo anayasema mama na kuyasimamia, ninyi kama wasaidizi wake kwa maana ya Waziri na watendaji wote myasimamie kwa vitendo, ndiyo tutapata matokeo ambayo tunayakusudia. Sasa ushauri wangu uko katika mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, kuhusu Kodi ya Majengo, tumekuwa na maelekezo na taratibu nyingi sana kuhusiana na Kodi ya Majengo. Huko nyuma, Halmashauri za Wilaya zilikuwa zinakusanya Kodi ya Jajengo, Serikali ya Awamu ya Tano ilipoingia madarakani ikachukua tozo hizi ikaipa TRA. TRA wakapambana nayo ikawashinda kwa sababu hawakuwa na uwezo lakini pia ilikuwa ni ngumu kuikusanya. Sasa leo mapendekezo yanakuja, tozo hii ya Kodi ya Majengo, ikatwe kutokana na Luku za nyumba. Unaponunua umeme, unakatwa kodi. Niwaambie kwamba, nadhani hili siyo jambo jema, linahitaji kutazamwa tena kwa upya. Kwa sababu tunajua watu wenye majengo huwa ni wachache na wanaolipa kodi mara nyingi ni wapangaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wamepanga. Akipanga anamlipa mwenye nyumba kodi yake, lakini suala la umeme linabaki kwake yeye mpangaji. Kwa hiyo, mwisho wa siku utekelezaji wa tozo hii inaenda kumfikia mpangaji na sio yule mwenye nyumba. Wenye nyumba ni wachache; ndiyo wapo, lakini anayenunua Luku ni yule mpangaji. Kwa hiyo, ni jambo la kutazama kwa upya ili kuhakikisha tozo hii iwafikie kweli wenye nyumba na sio wapangaji. Kwa sababu tunaelewa miji mikubwa watu wengi ni wapangaji. Miji kama Dar es Salaam watu wengi ni wapangaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye nyumba moja siku hizi ni utaratibu hata nyumba za biashara, kila mtu ana mita Luku yake, anajaza umeme wake mwenyewe. Sasa unaweza kukuta nyumba moja ina Luku karibia 10. Ina maana hawa wote wanatakiwa walipe kodi ya majengo, wakati wao ni wapangaji tu, mwenye nyumba yupo, anapokea kodi yake ya pango, halipi kodi nyingine yoyote. Kwa hiyo, ni vyema sana hili jambo likatazamwa kwa upya tukaondoa huu utaratibu kwa sababu unaenda kumkandamiza yule mpangaji na sio yule mwenye nyumba.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la pili; mnaweka ongezeko la shilingi 100 kwenye tozo za mafuta. Tunafahamu impact ya kuongeza tozo kwenye mafuta. Umeshakuwa ni utamaduni; ukiongeza tozo kwenye mafuta, kila kitu nchini kinapanda. Hii shilingi 100 tunayoongeza hapa mwezi Julai kila kitu tutakachokishika dukani kitakuwa kimepanda bei; impact yake ni kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa impact ya hii lazima itazamwe, naelewa lengo ni zuri, kwamba hizi fedha zipelekwe TARURA kwa ajili ya ujenzi wa barabara zetu kule vijijini; jambo jema kabisa, kwa sababu tunajua mwisho wa siku matokeo ya kuwa na barabara nzuri. Wakulima watapeleka mazao yao sokoni, barabara zitapitika, wanaotaka huduma za afya watapita kwenye barabara zinazopitika. Lakini hii impact ya pili ya kuongeza kodi ambayo itasababisha mfumuko wa bei ni lazima itazamwe kwa upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, kama utatuhakikishia you can control mfumuko wa bei, it’s okay, ni sawasawa. Kama hilo litawezekana, basi hizi fedha ambazo zitatozwa kwa ajili ya TARURA, kwa ajili ya ujenzi wa barabara zetu vijijini ziwe ring fenced kama zilivyo fedha za REA. Hapo ndiyo tutaona matokeo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashauri kwamba hizi fedha za TARURA ziwe ring fenced zitumike kwa makusudio hayo yaliyokusudiwa ili matokeo yake tuweze kuyaona kwa barabara zetu kupitika kwa kadri inavyotokea kwa mwaka mzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo linguine la mwisho; umuhimu wa sekta binafsi katika kujenga uchumi. Tunatambua uchumi wa nchi sekta binafsi nayo ni muhimu sana, lazima iwekewe mazingira mazuri, mazingira wezeshi, itazamwe ili iweze kuchangia katika uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mmoja; kulikuwa kuna viwanda mbalimbali hapa nchini ambavyo vimeanzishwa na ama ni wawekezaji au ni wazawa, lakini viwanda vingine vimekufa kwa sababu ya mambo mengi ambayo yanasababisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, kulikuwa kuna viwanda vya matrela. Miaka 12 iliyopita tulikuwa tuna viwanda visivyozidi 12, lakini hivi viwanda leo vimekufa, havipo tena. Kwanza, ajira imepotea, lakini hivi viwanda havijaweza kuwa endelevu kwa sababu ya mazingira mengi na mbalimbali, na moja wapo ni kwamba haya matrela yanaagizwa kutoka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni vyema Serikali ikatazama namna gani ya kutengeneza mazuri, kwanza kwa kuhakikisha kwamba hivi vifaa vinavyokuja kutoka nje, vinavyoagizwa, kwa maana ya matrela, na yenyewe iwekewe kodi kubwa ili ku-discourage zinazotoka nje na kuweza ku-encourage viwanda vya ndani vinavyotengeneza matrela na kuhakikisha kwamba kwa kufanya hivyo maana yake tutaongeza ajira, tutachangia kwenye pato la nchi kwa maana ya uchumi, lakini kuona namna gani kwamba tunaongeza ujuzi kwa Watanzania wetu, waweze kuwa na ujuzi ambao utatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye suala hili la viwanda vya matrela; ukiagiza gari dogo unatozwa ushuru wa asilimia 25, haya matrela yakiagizwa ushuru asilimia 10. Sasa lazima tuone namna ya ku-balance. Kama zote zinakwenda asilimia 25 ili ku-discourage ili kusaidia viwanda vyetu vya ndani, na hata wakati mwingine tufikirie namna ya kutoa ruzuku kwa viwanda vya ndani kwa sababu itachangia uchumi wa nchi, ajira na kukuza pato la mtu mmojammoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu wa mawazo kwa Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2022/2023. Ni ukweli usiopingika kwamba suala la mafanikio ya Mpango wowote ule ni uhakika wa upatikanaji wa fedha kwa ajili ya kugharamia mpango husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kitabu cha Waziri ameonyesha kabisa kwamba Mpango huu utagharamiwa na vyanzo vingi ambavyo vimetajwa ikiwemo mapato ya ndani, mikopo, misaada na kadhalika. Sasa ni vema Serikali ikajipanga kuhakikisha mapato ya ndani au makusanyo ya ndani yanaimarishwa na ili tuondokane na mawazo ya kukopa kupitiliza, tafsiri yake ni nini? Ni kwamba kukopa hakukatazwi, ni kawaida, lakini tusikope kupitiliza mwisho wa siku mzigo unauelemea Serikali na wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishauri Serikali kwamba ni lazima tuweke mikakati ya kuimarisha mapato ya ndani kudhibiti mianya ya ukwepaji wa kodi, kuhakikisha ulipaji wa kodi unafanyika kwa uhakika na kuondoa misamaha ya kodi isiyokuwa ya lazima. Kwa kufanya haya na mengine mengi, tutaenda kuimarisha makusanyo ya ndani na hatimaye haya ambayo yametajwa katika Mpango yatafanikiwa kutekelezwa kwa kutegemea kiwango kidogo cha mikopo, lakini kikubwa kitatokana na uhakika wa mapato yetu ya ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia ripoti ya CAG na tafiti mbalimbali zilizofanywa, hapa Tanzania tuna upotevu mkubwa wa mapato katika mambo tisa kwa uchache nikiyataja. Jambo la kwanza, kwenye sekta isiyo rasmi au wengine wanaita uchumi holela, tunapoteza takriban shilingi trilioni 2.8. Hoja ya pili, kukosekana kwa ufanisi kwenye Serikali za Mitaa katika ukusanyaji wa mapato, tunapoteza shilingi bilioni 50. Mamlaka za Umma kushindwa kutoa risiti za kielektroniki tunapoteza shilingi bilioni sita. Kama haitoshi, upungufu katika kufuata taratibu za kodi kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa na sekta za Umma, tunapoteza shilingi bilioni 14.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine ya tano ni kutokulipwa kwa malimbikizo na madeni mbalimbali, inaifanya Serikali ipoteze shilingi bilioni 113. Hii ni kwa mujibu wa ripoti za CAG na research zilizofanywa Action Aid ambao wametumia takwimu mbalimbali ikiwemo NBS. Kama haitoshi, kuna rufani za kodi ambazo hazijaamuliwa. Kuna hizo ambazo ziko za Barrick na wengineo, lakini mbali na hiyo, kuna shilingi trilioni tatu ambayo tunaipoteza ambayo maamuzi yake hayajaamuliwa. Kama haitoshi, kuna marupurupu ya kodi yenye madhara ya shilingi bilioni 153 ambayo nayo hayakusanywi. Kama haitoshi kuna mzunguko wa fedha haramu au illicit financial flows, tunapoteza shilingi trilioni 2.7 na la tisa, ni mapungufu ya makusanyo ambapo tunapoteza shilingi trilioni 1.4. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa takwimu hizi na figure nilizozitaja, ni kwa hakika kama Serikali ingeweka mkazo katika maeneo haya na mengine mengi ambayo sijayataja, kwa hakika suala la kukopa ili kuhakikisha mipango yetu inatekelezwa, tusingeliona kama ni jambo kubwa au la muhimu sana. Ni kwa kufanya mipango madhubuti, mipango sahihi sera sahihi, sera rafiki mambo yote ambayo yatahakikisha makusanyo ya ndani yanafanyika ipasavyo na haya ambayo tumeyaweka kwenye mipango na ugharamiaji wa Mpango kwa ujumla wake, unafanikiwa kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo yanasemwa muda mrefu hapa Bungeni na sijui kwa nini Serikali inakuwa nzito kutekeleza au kuyasimamia baadhi ya mambo.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Halima.

T A A R I F A

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nampa Mheshimiwa Paresso taarifa tu kuwa hoja yake hiyo ya mapato na kutoa ushauri kwa Serikali kuweza kupata vyanzo vingine mbadala; kwa taarifa ya Wizara ya Fedha kwa mfano, inasema kwa mwaka 2020/2021 huu mwaka ambao ndiyo tunamalizia, Serikali imeweza kukusanya kwa vyanzo vyote yaani ukizungumzia TRA, ukizungumzia Halmashauri zetu, ukizungumzia makusanyo yasiyo na kodi, yote yaani lile kapu lote, ni shilingi trilioni 20 tu ambazo zinaweza zikafanya mambo basically matatu; kulipa deni la Taifa shilingi trillioni 10, kulipa mishahara shilingi trilioni nane na vipesa vile vi-OC vile Other Charges.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, anachokizungumza ni sahihi kwamba basically miradi yetu yote ya maendeleo pamoja na kununua yale madege tunanunua kwa pesa za mikopo. Kwa ushauri wako, inakupa taarifa ili u-boost pale ambapo unashauri, vyanzo vingine tunaweza tukapata wapi? Ni hilo tu. (Makofi)

MWENYEKITI: Ilikuwa ni taarifa Mheshimiwa Cecilia, unaipokea?

MHE. CECILIA D. PARESO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naipokea taarifa hiyo. Naamini kabisa kwamba…

MWENYEKITI: Ngoja kidogo Mheshimiwa Cecilia, unapewa taarifa nyingine pia.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Nilitaka niwape taarifa kwamba ni utaratibu wa uendeshaji wa kiuchumi hata ngazi ya familia; unachukua kipato chako kile, unakifanyia simulation, unakichukua kwa mkupuo, halafu unatekeleza jambo kubwa; unaanza kurejesha kupitia jambo kubwa ulilotekeleza na jambo kubwa lile ambalo unakusanya. Kwa hiyo, siyo jambo la kwamba hakuna mapato ndiyo maana tunakopa. (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa kwa Waziri.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Cecilia ndiyo mchangiaji, endelea. (Kicheko)

MHE. CECILIA D. PARESO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Taarifa yake siipokei. Ni hivi, yaani kukopa siyo dhambi na wala haikatazwi, lakini unakopa kwa ajili ya nini? Unakopa uende kufanya nini ili utakachokopa kirejeshe on time na ili uendelee kukopa na hicho utakachokifanya, matokeo yake yaonekane? Mbona ni kitu rahisi tu hiki na kinaeleweka tu. Mimi sio mchumi, lakini naielewa tu kwa namna hiyo, kwamba ni kitu ambacho kinaeleweka tu. Sasa… anyway, usinitoe kwenye hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hivi, mambo yote ambayo nimeyashauri hapa, ya kuimarisha makusanyo ya ndani na yawe endelevu, kudhibiti upotevu wa mapato, kuiwezesha TRA kwa maana ya rasilimali watu na vyote vinavyowezekana ili waweze kwenda kuhakikisha ukusanyaji wa kodi na mambo mengine yanafanyika, lakini pia kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara. Kwa sababu ukiweka mazingira rafiki, mwisho wa siku kodi inalipika bila kuwa na nguvu au kushurutishana, bila kuwa na hiyo kwamba nikupe risiti au nisikupe risiti. Haya yote yanafanyika kwa kuhakikisha kwamba huu udhaifu tuliouataja unaenda kuimarishwa ili tukuze ukusanyaji wa mapato ya ndani tuepukane na kukopa kunakopitiliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo napenda kuchangia kwa haraka haraka ni suala la deni la Taifa. Hapa tunapoongea, mpaka Septemba mwaka huu 2021, taarifa za BoT zinaonyesha kwamba kuna ongezeko la deni la Taifa ambapo mikopo kwa deni la Taifa la nje imefikia shilingi trilioni 59 na deni la ndani imefikia shilingi trilioni 18. Kwa hiyo, jumla yake inafanya deni la Taifa kufikia shilingi trilioni 78. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni hali ambayo inatisha, ni lazima tuhakikishe tunakopa kwa vitu ambavyo kwa kweli ni lazima sana tukope na siyo vinginevyo. Kwa sababu tunakoelekea sasa hivi, hii mikopo yote ikiiva, maana yake makusanyo yote tutakayoyapata ya kwanza tunaanza kulipa madeni. Tutafika mahali hata mishahara tutashindwa kulipa kwa sababu madeni yameiva kila kona tulikokopa. Hii ni hatari sana kwa uhai wa nchi na wananchi kwa ujumla. Sasa Awamu ya Tatu iliacha deni la shilingi…

MHE. CHARLES J. MWIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

SPIKA: Taarifa, nakuruhusu mtoa taarifa.

T A A R I F A

MHE. CHARLES J. MWIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpe taarifa mzungumzaji, Mheshimiwa Paresso kwamba usiwe na hofu na kukopa. Tunapanga kukopa ili kuwekeza na kutokana na kuwekeza tupate na matokeo yake. Unapozungumza miundombinu wezeshi na saidizi inaleta tija kwa maendeleo ya nchi. Wale wasiozijua ndege wanaweza kuzibeza, lakini sisi tunaosafiri na ndege, tunajua maslahi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yangu ya Ardhi inaandika paper kuja Serikalini, tunataka Serikali ikope shilingi trilioni mbili iweke kwenye sekta za kiuzalishaji, the productive sectors tuweze kuuza chakula dunia nzima na kufuga samaki na kuuza dunia nzima, ambapo soko la samaki ni dola bilioni 235. Tunataka tuingie kule. Kwa hiyo, kama fursa ipo, usiogope kukopa. Kampuni zote zinakopa na nchi zinakopa. (Makofi)

MWENYEKITI: Taarifa hiyo Mheshimiwa Cecilia Paresso.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Taarifa yake siipokei na narudi kule kule na napenda anielewe vizuri na Serikali inielewe, kwamba kukopa siyo dhambi na haikatazwi, lakini unakopa ufanye nini ili kuwepo na mapokeo ambayo utaweza ku- service mkopo ule ili mambo mengine yasikwame.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaongelea habari ya Deni la Taifa na tena nafikiri mliite Deni la Taifa siyo la Serikali, kwa sababu kwenye vitabu humu wameandika Deni la Serikali, ni Deni la Taifa ili Watanzania wajue. Deni la Taifa leo tunapoongea ni shilingi trilioni 78, sijui ni bajeti za Wizara ngapi tulizonazo, sijui ni bajeti ya nchi yote kwa ujumla.

Sasa ninachoshauri ni kwamba, tuangalie tunakopa kwa ajili ya nini, kwa masharti yapi, kwa kufanyia nini na kwa matokeo yapi? Haya ni mambo ambayo tunayasema, tutashauri, na tutaendelea kushauri utekelezaji…(Makofi/ Kicheko)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili, Ahsante sana.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kidogo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji na kufanya maamuzi kwenye mambo haya siyo Biblia wala siyo Quran ni mambo ambayo yanabadilika kulingana na wakati na kulingana na uhitaji husika. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja za Kamati zilizoko mbele yetu. Hali ya upatikanaji wa dawa hapa nchini katika hospitali zetu, vituo vya afya na zahanati kwa ujumla ni mbaya na dawa hazipo na wananchi hawapati huduma zinazostahiki. Tunafahamu tuna bohari ya dawa ambazo kazi yake ni kununua na kusambaza dawa na sasa tumeipa jukumu lingine, tumebadilisha sheria ya kuanzisha viwanda vya kutengeneza dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba hii MSD imezidiwa. Mara nyingi hapa Bungeni tumekuwa tukisema tu Serikali ina idai MSD, labda ufanisi wa MSD hauonekani kwa sababu inaidai fedha nyingi. Mimi naona kama hicho ni kichaka tu cha kujifichia humo. Ni kweli kwamba inaidai Serikali na ripoti mbalimbali za CAG zimeonyesha, lakini MSD yenyewe pamoja na kidogo kinachopatikana, bado mfumo wake wa usambazaji wa dawa ni hafifu wa kizamani na hautoi matokeo yale ambayo wananchi wanayatarajia na huduma kule kwenye vituo vyetu, hazipatikani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hata Naibu Waziri wakati anajibu swali hapa akasema shida siyo fedha, fedha zipo lakini shida nadhani nyingine wanaijua. Kwa hiyo, nadhani iko haja sana ya kufanya kufumua MSD na kuiunda upya kwa kuangalia mahitaji ya leo na kuweka mfumo ambao usambazaji wa dawa utatosheleza na utafika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, kwenye Mkoa wangu wa Arusha, sasa hivi MSD wanapita kwenye vituo wanapeleka dawa. Wananchi wanaona gari limefika, linashusha dawa, lakini wanashusha dawa za wiki moja tu, magari yanaondoka. Hata hilo gari halijafika kwenye Bohari Kuu, huku nyuma dawa zimeisha na mpaka warudi, siyo leo. Kwa hiyo, tusitegemee tena wananchi watapata huduma. Kwa hiyo, ni lazima tuangalie namna gani tutahakikisha wananchi wanapata dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine, tuliambiwa kwenye Kamati juzi; leo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kuna uhaba mkubwa sana wa hizi blood bags, mifuko ya kuwekea damu; na wenyewe wamekiri kabisa pale Muhimbili hakuna, lakini maeneo mengine nchini inapatikana, iko mpaka ya ziada. Sasa unajiuliza, kuna nini? Maana yake kuna tatizo la mgawanyo na usambazaji na usimamizi wa dawa pamoja na vifaa vyote vya dawa hapa nchini. Kwa hiyo, iko haja sana ya kuitizama MSD na kuifumua na kuhakikisha kwamba inafanya huduma ambayo inatakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, hapa juzi juzi tulisikia tamko la Waziri kuhusiana na kufunga maduka yote ya dawa zilizoko karibu na hospitali au vituo vya afya au vinginevyo; na amerejea sheria ambayo tuliipitisha hapa Bungeni. Hiyo sheria inaonesha kabisa kwamba duka la dawa kwenye hospitali itakaa mita 500; kwenye ngazi ya mkoa itakaa mita 400; kwenye ngazi ya wilaya itakaa mita 300; kwenye vituo vya afya na zahanati itakaa mita 200; na akaagiza kwamba ziondoke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hili tamko siyo sahihi, kwa sababu kwanza haya maduka ni Serikali wenyewe mmesaidia kuyafanya yashamiri na kustawi, kwa sababu maduka yetu ya dawa zilizopo ndani ya hospitali hakuna dawa. Kwa hiyo, mwananchi hayuko tayari mgonjwa wake afe kwa sababu hakuna dawa ndani ya hospitali eti asiende kutafuta kwenye duka la dawa. Kwa hiyo, nyie wenyewe mmesaidia kuyafanya yashamiri na hawa watu wanaendesha biashara kihalali, wako kihalali, mmewapa vibali wenyewe, wanalipa leseni, wanalipa kodi, leo mnawaambia waondoke. Hilo siyo suluhisho. Kuwaambia maduka haya yaondoke, siyo suluhisho la kuhakikisha dawa zinapatikana kwenye hospitali zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotakiwa ni kuimarisha MSD. Kuhakikisha MSD inatoa dawa zote na kwa wakati katika hospitali zetu. Hospitali zetu, vituo vya afya na zahanati zikiwa well equipped na dawa zote, haya maduka automatic yatapotea, hayatakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani Serikali kwenye hili jambo muiache kama ilivyo. Mwananchi yeyote hayuko tayari kuona eti mtu wake anafariki hapa kwa kukosa dawa asiende kutafuta dawa kwenye duka la dawa kwa sababu Serikali imetoa tamko, haiwezekani. Kwa hiyo, ni Serikali kuhakikisha MSD inaimarishwa, inasambaza dawa zote muhimu kwa wakati na wananchi wanapata dawa ambazo zinatakiwa kulingana na ugonjwa ambao anaugua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni upungufu wa watumishi wa afya. Ripoti mbalimbali za CAG zimeonyesha tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi wa afya. inakaribia 52% ya watumishi wa afya ambao wanahitajika waajiriwe ili huduma muhimu na stahiki ziweze kutolewa kwenye vituo vyetu vya afya na katika maeneo yote ambayo tunatoa huduma za afya. Hata hivyo, bado ajira hizi hazijatangazwa. Maana yake ni kwamba, huku tuna changamoto ya dawa, huku hatuna watumishi; hivi mnawataka nini Watanzania hawa? (Makofi)

Mheshimwia Mwenyekiti, kama tunaweza kukopa fedha tukajenga SGR, tukajenga sijui Mwalimu Nyerere Stiegler’s Gorge, kwa nini tusiwekeze kwenye afya za Watanzania? Hata hiyo SGR na Stiegler’s Gorge tutakuwa tunamjengea nani kama Watanzania wote watakuwa wagonjwa, hakuna dawa? Itakuwa ni kazi bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali iliweza kufanya maamuzi yale ikaweza kutafuta fedha kujenga SGR, kujenga Stiegler’s hivyo hivyo fanyeni uamuzi sahihi…

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Mollel.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sipingani na mawazo mazuri ya Mheshimiwa Mbunge, lakini nilitaka tu nimpe taarifa kwamba unapoajiri, unaajiri kulingana na ukuaji wa uchumi wako na unapokopa, unasisimua uchumi ukue ili uweze kuajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa kwamba kwa mwaka huu tu tayari tumeruhusiwa kuajiri watu 21,000. Hata hivyo, ukikopa ukawekeza hizo fedha, kuna maeneo matatu ya kuwekeza ili uchumi ukue na uweze kuajiri wengi; uwekeze kwenye human resource capital, ambayo ndiyo imewekezwa sasa hiyo shilingi bilioni 1.3 kwenye elimu, afya na sehemu nyingine ambazo zinaenda kukuza na kukuza pato letu la Taifa; tunawekeza kwenye teknolojia na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakubaliana na mawazo yake, lakini anachokifanya Mheshimiwa Rais ni hicho hicho anachokisema yeye. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, pokea taarifa.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Tunatambua kwamba uchumi hauwezi kuwa muhimu sana kuliko afya za Watanzania. Yaani inaweza ikawa inaenda sambamba, lakini naongelea hapa afya za Watanzania kwa ujumla wake. Mnaweza mkawa mmetoa hizo ajira, lakini bado uhitaji ni mkubwa. Si tuko kule tunaona kwenye vituo vyetu vya afya, zahanati na kila mahali.

Kwa hiyo, nadhani waipokee kama ushauri na Naibu Waziri utapata nafasi, utakuja kueleza hayo na tutaendelea kushauri na ndiyo wajibu wetu mkubwa wa Wabunge hapa Bungeni.

MWENYEKITI: Sasa endelea kuchangia Mheshimiwa Paresso baada ya kupokea taarifa nzuri ya Serikali.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nasema suala la watumishi wa afya, ajira ni muhimu na ninaendelea kulisisitiza kwamba ni muhimu Serikali iajiri kuhakikisha Watanzania wanapata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naeleza kwamba kama tunaweza kuwekeza nguvu kubwa kwenye masuala ya kiuchumi kwa maana SGR, Stiegler’s, hawa Watanzania ambao wanategemewa waje watumie hayo kwa kuwa na afya njema, kama hatujawaandalia mazingira ya kuwa na afya njema kwa kuhakikisha dawa na huduma katika hospitali zetu zinapatikana inavyotakiwa, itakuwa ni kazi bure. Tutakuwa na Taifa la watu ambao ni wagonjwa, hakuna dawa. Tutakuwa na Taifa ambalo haya tunayoyatengeneza, hayatakuja kutumiwa kwa sababu watu wote wanaumwa hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachoshauri ni kwamba uwekezaji kwenye sekta ya afya kwa kuhakikisha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba watumishi wa afya wa kutosha kwenye sekta hii, itiliwe mkazo sawa sawa na mkazo ule ule kwenye sekta nyingine ambazo tunaziona kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo,...

MWENYEKITI: Kengele ya kwanza Mheshimiwa. Endelea, hiyo ni ya kwanza itagonga ya pili. Malizia.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala lingne kuhusu mtaala wa elimu ambao tunaufanyia marekebisho kwa sasa. Kama ambavyo Serikali imesema na kama ambavyo ripoti yetu imeonyesha, ni kwamba tunatarajia mtaala huu utakuja kuanza utekelezaji 2026. Najiuliza swali moja; Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Marehemu Hayati Dkt. Magufuli, kipindi hicho alitoa agizo kuhakikisha tunaingiza somo la historia kwenye mtaala wetu wa elimu na mtaala ufanyiwe maboresho. Jambo hilo lilitekelezwa within two months or three months na ikafanyika na Wizara ikatengeneza vitabu, ikachapisha, wanafunzi wakaanza kufundishwa, ikatekelezeka. Leo kwa nini tunashindwa kuhakikisha kwamba hii sera yetu ya elimu inayofanyiwa maboresho inaenda kutekelezwa on time? Kwa nini mpaka 2026? Kuna nini hapa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kinachoonekana ni kwamba hakuna utayari au utashi wa kuhakikisha suala hili linafanyika. Tukumbuke kwamba dunia ya leo inakimbia, sisi inawezekana tuko nyuma sana. Huko duniani watu wanakimbia, ugunduzi unaendelea, mambo yanaboreka kila siku. Profesa hapa ameeleza vizuri sana, kama tukiwa wagumu, tukiwa na urasimu wa kufanya mabadiliko na kukubali mabadilika kwa wakati…

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Nusrat Hanje.

T A A R I F A

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba anachokisema ni ukweli na hata Sera ya Sayansi na Teknolojia ambayo ilitakiwa iwe Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu imeishia kwenye Sera ya Sayansi na Teknolojia, lakini pia ni ya mwaka 1996, ina miaka 28. Hata Sheria ya COSTECH ni ya mwaka 2000. Yaani sera yenyewe tunayoizungumzia maana yake itakuwa outdated kabla hata haijaanza kutekelezwa, kwa sababu lifespan ya sera ni 10 years. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Paresso, taarifa hiyo.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nimeipokea taarifa hiyo nzuri sana na naamini pia wameisikia. Hoja yangu hapa ni kwamba, sijui kwa nini Wizara wanakuwa wagumu au wazito na kunakuwa na urasimu mkubwa. Najua, inaweza ikawa ni mabadiliko ambayo yanahitaji mambo mengi, lakini tujaribu, tufanye huo uthubutu, tuhakikishe kwamba Sera ya Elimu tunaitekeleza kwa wakati na tuendane na dunia na teknolojia ya leo, kuhakikisha kwamba tunazalisha na tunatoa wataalam ambao wanakubalika duniani katika kuingia kwenye soko la ajira na kuisaidia nchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hayo tu, nakushukuru sana, na naunga mkono hoja ya Kamati.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya TAMISEMI na Utawala Bora na Utumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kueleza kwamba ni ukweli usiopingika hali za Halmashauri zetu nchini kwa ujumla wake ni mbaya sana. Halmashauri hizi zina hali mbaya kwa sababu nyingi zimekuwa tegemezi na kwa asilimia kubwa zinategemea fedha kutoka Serikali Kuu. Halmashauri zetu hizi pia vyanzo vile muhimu ambavyo vingewezesha mapato ya Halmashauri zetu kuongezeka, kwa kiwango kikubwa vimechukuliwa pia na Serikali Kuu. Kwa hiyo, tumeziacha Serikali zetu za Mitaa katika hali ngumu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine kuna uhaba mkubwa wa watumishi katika Serikali za Mitaa kwa maana ya rasilimali watu. Takwimu zinaonesha tuna uhaba wa watumishi 43,560 katika idara 470 za Halmashauri zetu nchini, huu ni upungufu mkubwa sana. Kama kuna upungufu huu mwisho wa siku hata ufanisi wa fedha zinazopelekwa unakuwa hauonekani au haupo kabisa au ufanisi unakuwa kwa kiwango kidogo sana.
Kwa hiyo, ni muhimu sana Serikali ikaangalia ni namna gani wanakwenda kupunguza uhaba wa watumishi walioko katika Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine unapoongelea suala la Serikali za Mitaa huwezi kuwaacha Madiwani pembeni. Ni kwa muda mrefu Serikali mmewatelekeza Madiwani si kwenye maslahi, si kwenye kujengewa uwezo, Madiwani maslahi yao yanaboreshwa kwa kiwango kidogo sana. Ukiangalia sisi Wabunge hatuna utofauti sana na Madiwani lakini tunawaacha Madiwani na sisi tukiwa Bungeni muda mrefu wanaotufanyia kazi kwa kiwango kikubwa na kutusaidia ni Madiwani. Ni muhimu sana Serikali ikaangalia namna gani maslahi ya Madiwani yanaboreshwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini si maslahi tu, wakati wa awamu iliyopita walifuta mafunzo (capacity building) kwa Madiwani. Hivi unampeleka Diwani akamsimamie Mkurugenzi na watendaji wake ambao wao ni wataalam wa mambo fulani fulani halafu Madiwani wetu wamechaguliwa tu kwa kigezo cha kusoma na kuandika, hana ujuzi wowote, baadhi lakini wako wengine ambao wana ujuzi lakini walio wengi hawana ujuzi huo, hivi kwa nini Serikali isiirudishe ile programu ya kuwajengea uwezo Madiwani kwa kuwapatia mafunzo. Mimi nilikuwa Diwani, nakumbuka kulikuwa kuna programu ya kuboresha Serikali za Mitaa, tulikuwa tunapelekwa mafunzo ya miezi sita lakini inakwenda kwa awamu, ilitusaidia kutujenga na kusimamia zile fedha zinazopelekwa. Kwa hiyo, ni muhimu pia mkalitazama hili muone namna gani Madiwani wanarudishiwa hizo programu za kujengewa uwezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia kuhusu TAMISEMI ni udhaifu mkubwa ulioko katika usimamiaji wa Bajeti na Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa. Kuna udhaifu mkubwa sana, udhaifu huu unaendana na bajeti zilizoidhinishwa kutokufuatwa na hizi bajeti wakati mwingine hazifuatwi kwa sababu ya matamko ya viongozi mlioko ngazi za juu na mlioko katika Serikali Kuu. Mfano, Halmashauri 34 zimetumia kiasi cha shilingi bilioni 33 kwa ajili ya ujenzi wa maabara. Hakuna mtu anayepinga au anakataa umuhimu wa maabara, umuhimu wa maabara unajulikana lakini ujenzi huu na fedha hizi zimetokana na tamko lililotolewa na Rais bila kuangalia wakati huo anatoa tamko kwenye bajeti za Halmashauri za Wilaya fedha hizi zipo? Kwa hiyo, inaonesha kuna shilingi bilioni 33 zimetumika kinyume na bajeti eti kujenga maabara katika shule zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine, kuna takriban upotevu wa shilingi bilioni nane kwa ajili ya malipo yaliyofanywa na Serikali za Mitaa bila kuwepo na nyaraka za malipo. Pia kuna Halmashauri 62 zimefanya malipo ya shilingi bilioni 1.4 kinyume na vifungu vilivyopitishwa katika bajeti. Sasa kama Serikali hizi za Mitaa hazifuati bajeti ambayo imejiwekea hakuna sababu ya kupitisha bajeti au kama kuna matamko yanayotolewa bila kuangalia uhalisia wa Serikali zetu za Mitaa hakuna sababu ya kuwa na Serikali za Mitaa kama hatutambui na kuthamini yale ambayo yanayopitishwa katika bajeti zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma ripoti ya CAG anasema watekelezaji wa miradi 76 walifanya matumizi nje ya bajeti ya kiasi cha shilingi bilioni 4.6. Yote ni kukiuka bajeti waliyojiwekea, yote ni kukiuka Sheria ya Fedha ambayo ipo. Wanasema matumizi mengine yalifanywa nje ya bajeti na yameongezeka, CAG anasema matumizi nje ya bajeti yameongezeka kwa asilimia 224. Kwa hiyo, haya ni mambo ya kuyaangalia na kuyasimamia kuona yanaondoka katika Serikali zetu za Mitaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie eneo lingine la elimu bure. Mmesema mnatoa elimu bure, lakini nilidhani mngepaswa kujiridhisha na kuangalia hivi ni kweli mnaweza kutoa elimu bure au mlikurupuka tu mkachukua Ilani yetu na yenyewe mkaweka kwenye Ilani yenu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivyo, kuna watu wamefanya tafiti, wanasema ili uweze kutekeleza elimu bure unahitaji takriban shilingi bilioni 715 kwa mwaka mmoja wa fedha. Ili uweze kutekeleza elimu bure maana yake unahitaji mambo makuu manne; jambo la kwanza ni kutoa ile ruzuku ambayo ilikuwa inatolewa ya shilingi 10,000 kwa shule za msingi na shilingi 25,000 kwa shule za sekondari. Kama ile ruzuku mmeamua kuitoa kwa sababu mnasema ni elimu bure maana yake Serikali inahitaji karibia shilingi bilioni 130 kwa shule za msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, kama mnaondoa ada ya shilingi 20,000 kwa watoto wa sekondari, Serikali inahitaji kuwa na shilingi bilioni 31.5 ili kufidia ada hiyo. Hivi hizi fedha hizi mnazo? Si huwa mnasema kasungura kadogo? Safari hii kamenenepa? Nadhani mnapaswa kuangalia haya mliyoyasema ya elimu bure hivi mnakwenda kutekeleza? Halafu mmetoa Waraka mwingine Na. 5 wa elimu mnasema kama wanataka wapate kibali kwa Mkuu wa Mkoa, sasa kwa nini hizi contradiction, si mmesema elimu bure? Basi acheni bure mbebe huo mzigo, mtafute fedha hizi mwende kutekeleza elimu bure ambayo mnataka kuitekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kwa haraka ni kuhusu Mfuko wa Vijana na Wanawake. Waheshimiwa Wabunge wengi tunachangia kwamba tuhakikishe Serikali za Mitaa zinatenga ile 10 percent kwa ajili ya Mfuko wa Vijana na Wanawake lakini lazima kidogo twende mbali ya hapa. Mifuko hii ukiangalia mwongozo wake na mwongozo huu ulipitishwa na Bunge hili mwaka 1991, ni mwongozo wa zamani ambao hauendani na uhalisia wa leo.
Katika Bunge la Kumi niliuliza Swali Na. 379 kuitaka Serikali i-review ule mwongozo wa kuanzisha Mifuko ya Vijana na Wanawake, ni mwongozo wa zamani sana kwa sababu unasema kikundi cha watu watano watapewa mkopo wa shilingi 500,000. Hivi unawapa mkopo wa shilingi 500,000 kwa watu watano, shilingi laki moja moja inasaidia nini, haisaidii kitu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ni vizuri mkaangalia tena kwa upya namna gani ya kuu-review mfuko huu uendane na hali halisi iliyoko katika maeneo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye Wizara ya Utumishi na Utawala Bora, kuna Mfuko wa TASAF. Mfuko wa TASAF ni mkopo kutoka World Bank ambao ni dola za Kimarekani milioni 200 lakini fedha hizi zinakwenda kupewa watu kwenye kaya, wanasema kaya maskini na kwenye kaya maskini wanaangalia vigezo mbalimbali kama kuna wategemezi na vitu kama hivyo na kwenye kila kaya range ya fedha hizi ni kati shilingi 20,000 mpaka shilingi 62,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka kuwakwamua watu wetu kutoka kwenye hali mbaya ya umaskini hivi ni kuwapa fedha mkononi? Kwa sababu ukimpa fedha mkononi itamsaidia nini? Kwa sababu hizo hizo Kaya maskini wakati mwingine hata mlo kwa siku ni taabu, ukimpa shilingi 20,000/= unamwendelezaje aondokane na huo umaskini? Kwa hiyo, ni muhimu mkaangalia hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kumekuwa na mifuko mingi ambayo mwisho wa siku hatuoni manufaa yake.
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka huu wa fedha 2016/2017, Wizara imeeleza kwamba inafanyia mapitio ya Sera ya Ardhi ya mwaka 1995. Mapitio haya yatakuwa hayana maana kama Wizara haitajikita kuimarisha mfumo wa utendaji wa vyombo vya usimamizi wa ardhi katika nchi hii. Hapa tunaongelea Serikali za Vijiji, pamoja na mabaraza yake ya ardhi maana yake hata kama ukiwa na sera lakini hujaviwezesha vyombo hivi ukavipa rasilimali fedha, ukavipa rasilimali watu, sera yao wanayokwenda kurekebisha itakuwa haina maana.
mamlaka hizi za usimamizi wa ardhi katika nchi yetu na kuimarisha mfumo mzima wa utendaji wa Wizara katika maeneo mbalimbali. Pamoja na marekebisho hayo ni muhimu tukaangalia masuala mazima ya wawekezaji au baadhi ya wawekezaji na viongozi na wanasiasa kuhodhi maeneo makubwa kinyume na taratibu au kuihodhi kwa kufuata utaratibu lakini wameya-damp na hawayaendelezi ni muhimu sana hili likatazamwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wawekezaji wengi baadhi yao wana-forge muhtasari wanalaghai Serikali zetu za Vijiji, wanahodhi maeneo na wanayatumia maeneo hayo kwenda kukopea benki na kudanganya au kudanganya kwamba wana mitaji lakini hawana mitaji, wanatumia ardhi hiyo kwenda kukopa benki wanafanya biashara nyingine wanatelekeza zile ardhi. Kwa hiyo, ni muhimu sana Wizara ikatazama kwa ujumla wake suala zima la hawa wawekezaji, baadhi yao wamekuwa ni wadanganyifu wakubwa wakitumia ardhi zetu vibaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna baadhi ya wawekezaji wanabadilisha matumizi ya ardhi kinyume na hati miliki zao zinavyoeleza, kuna wawekezaji wanapewa kwa ajili ya kilimo, anakwenda kubadilisha. Nimpe mfano Mheshimiwa Waziri, Wilaya ya Karatu, kwa taarifa ambayo tumeletewa kwenye Baraza la Madiwani kuna mashamba ambayo yanamilikiwa na wawekezaji, yametembelewa mashamba 18 ambayo yana jumla ya hekari 13,985 wengi wao mashamba haya wamepewa kwa ajili ya kilimo cha kahawa, lakini wako baadhi wamebadilisha matumizi wamejenga hoteli kubwa za kitalii, hatuna uhakika kama wamefuata taratibu za sheria za kuomba kubadili matumizi ya ardhi ile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya ardhi ile inaonekana ni kilimo, lakini wako wengine wamejenga hoteli za kitalii maana yake ni nini? Maana yake ni pia wanaikosesha Serikali mapato, anakwenda kulipa tu kwa sababu inaonekana hati yake ni ya kilimo lakini amejenga hoteli kubwa ya kitalii analaza wageni, anapata fedha za kutosha. Kwa hiyo, ni muhimu sana Wizara ikafanya uhakiki kutembelea mashamba, ambayo jumla yako mashamba 32 ndani ya Wilaya ya Karatu yakabaini ni watu gani ambao wamekiuka taratibu za kisheria katika umiliki wao wa ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia katika hao wawekezaji wenye mashamba 32, wako wengine wameyatelekeza mashamba, wako wengine wameyaacha, wamehifadhi halafu kuna wananchi wengi pembezoni pale hawana hata maeneo ya kuzika. Mheshimiwa Waziri ningetamani aje karatu aone. Yako mashamba yanamilikiwa na Wahindi, wananyanyasa watu, wanadiriki kuwaambia hata kaya zinazokaa pale, ni marufuku kuzaana eti kwa sababu wataongeza idadi, huu ni unyanyasaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa sana Mheshimiwa Waziri afike, aone jinsi gani wananchi hawa, hawana hata maeneo ya kuzikana sasa wananchi wanakuwa watumwa katika nchi yao, haiwezekani! Hatuwezi kuthamini wawekezaji, hatuwezi kuthamini watu hao tukawapuuza wananchi wetu ambao ni damu zetu. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, suala hili liondoke na wananchi hawa wapate haki yao, wapate maeneo angalau hata kuweza kuzikana katika nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka niongelee ni kuhusu migogoro ya ardhi. Migogoro hii ya ardhi imekuwepo kwa muda mrefu na migogoro hii mara nyingi ni kati ya wakulima na wafugaji, hifadhi na wananchi, vijiji na vijiji na kadha wa kadha kama ambavyo imeoneshwa katika hotuba yetu ya Kambi ya Upinzani. Pamoja na kwamba bado tuna migogoro lakini imepungua sana, lakini inawezekana ikaendelea kuibuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro hii pamoja na sheria tulizonazo, lakini ni lazima Serikali ijikite katika kuimarisha vyombo vya utatuzi wa migogoro ya ardhi na lazima Serikali iangalie namna bora ya kumaliza migogoro hii ya ardhi kwa njia shirikishi na kutumia mila na desturi za maeneo mbalimbali. Hatuwezi tu kusema wakati mwingine tunafuata sheria kama ilivyo, kwa sababu mkisema mnafuata sheria kama ilivyo, ndiyo mnaua watu, mnajeruhi watu, mnafukuza watu, wakati mwingine busara itumike kwa kutumia mbinu shirikishi ya kuondoa migogoro hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano migogoro ya wakulima na wafugaji inaweza wakati mwingine kusuluhishwa kwa kutumia, mila na desturi na njia shirikishi siyo unakwenda kusuluhisha migogoro hii kwa kuchimba sijui mitaro, sijui kwa kusema wasivuke huku, haiwezekani ni lazima mtumie njia shirikishi ambayo itaweza kuondoa migogoro ya ardhi katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala moja la umiliki wa ardhi. Wapo Watanzania wengi ambao hawana hati miliki na wako wachache ambao wana hati miliki. Sababu ambazo zinapelekea hili, wakati mwingine ni urasimu na mlolongo mzima wa kupata hati hizi, kuanzia kwenye Halmashauri zetu mpaka hizo Ofisi za Kanda ambazo zinatoa hati miliki. Pia, wakati mwingine kuna rushwa kwenye halmashauri zetu, Halmashauri kule kuna shida sana kwa hao Maafisa Ardhi. Hizi rushwa zinawanyima wananchi haki ya kupata ardhi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niishauri Serikali muandae programu maalum ya kuhakikisha mnakopesha wananchi, yaani kuliko mwananchi atafute fedha ya kuingia gharama ya hatua hizi mpaka apate hati, mnaonaje mkiwa na programu maalum, Serikali ikagharamia, mkawakopesha wananchi wakawa na hati zao, wakalipa kidogo kidogo mpaka akamilishe deni lile, ili tuhakikishe wananchi walio wengi wanapata hati, maana yake hati hizi wakipata mwisho wa siku wanalipa mapato, inakuwa ni sehemu ya mapato ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie jambo la mwisho, kuhusu ulipaji wa fidia pale ardhi inapotwaliwa. Jambo hili mmeeleza kwamba mmeanzisha Mfuko huu wa kutoa fidia ambayo itaanzia na bilioni tano. Ni muhimu sana Serikali ikawalipa wananchi fidia kwa wakati, ikawashirikisha wananchi katika…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Nianze mchango wangu katika kipengele cha kwanza kuhusiana na watumishi wa Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba watumishi wa umma ndiyo injini ya nchi. Kama ambavyo tunatambua umuhimu wa injini katika magari yetu vivyo hivyo watumishi wa umma ni muhimu katika nchi hii kwa sababu wao ndiyo wapanga mambo yote na watekelezaji wa mambo yote hapa nchini na bila wao hakuna mafanikio yoyote ambayo sisi wanasiasa kwa namna moja au nyingine tunaweza kujivunia nayo. Hivyo basi, hawa watumishi wa umma wanatakiwa kwa umuhimu huo kujengewa mazingira yote muhimu na rafiki ya kuhakikisha kwamba wanapofanya kazi zao wanafanya kazi katika mazingira ambayo yanaleta matokeo tunayotarajia sisi wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni pamoja na watumishi wa umma wote ambao wana-qualify kupandishwa madaraja na vyeo Serikali haina budi kuhakikisha watumishi hawa kwa wakati madaraja yao na vyeo vyao vinapandishwa. Tumesikia kupitia taarifa ya Waziri amesema kati ya Julai 2021 na Machi 2022 watumishi laki 190,781 walipandishwa vyeo na madaraja, lakini hajatuambia kati ya mahitaji mangapi. Huwezi tu kusema umepandisha hawa lakini hamjatuambia ni wangapi wana-qualify kupandishwa madaraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni vyema sana Waziri ukatuambia wanao-qualify ni wangapi na kwa awamu hii mmepandisha wangapi. Kwa hiyo tusijifiche kwa kutoa hizi takwimu tu zikaonekana ni nyingi kumbe uhitaji ni mkubwa sana huko kwa watumishi ambao wanapaswa kupandishwa vyeo na madaraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, uhaba wa watumishi wa umma, kama ambavyo nimeanza kwa kuelezea umuhimu kama kuna uhaba wa watumishi wa umma automatic ufanisi wa mambo katika nchi hii hauwezi kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema, mahitaji halisi ya watumishi wa umma hapa nchini ni milioni 1,232,089 lakini waliopo mpaka sasa takwimu zinaonyesha ni mia 679,995 kuna upungufu wa laki 558,134 sasa tuna upungufu wa laki 558 plus lakini ajira zilizotangazwa juzi ni 32,000 katika kada zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuone tu kwamba bado tuna uhitaji mkubwa sana wa watumishi wa umma. Swali linakuja hivi ni kwanini ni kwamba labda hatuna watumishi ambao ni qualified? Lakini si kweli. Kwa mujibu wa taarifa ya TCU wanaohitimu Vyuo Vikuu, nina takwimu hapa za miaka mitatu; 2018, hiyo ni Vyuo Vikuu tu sijachukuwa takwimu za vyuo vya kati, Vyuo Vikuu wanamaliza na kuingia kwenye soko la ajira ni 49,154 kwa mwaka 2018, 2019 ni 51,000, 2020 elfu ni 48,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba, kama tuna upungufu ukitaka kusema hatuna wanao-qualify sio kweli kwa sababu tafiti za TCU itakuonesha ndivyo sivyo; na maana yake kwa miaka mitatu tunazalisha wahitimu laki 148,853. Kati ya hao laki 148,853 wenye degree ya kwanza ndio wengi zaidi ambapo kwa mwaka 2020 tu tunatoa walio na degree ya kwanza 34,168. Katika ya hao 1,468 ambao wanaongoza ni wale waliosoma degree ya kwanza ya education, ambao kwa mwaka 2020 tu tumewatoa wahitimu 14,644, wa degree tu ya kwanza ya education. Halafu ajira tulizozitangaza kwenye specific elimu kwa maana ya walimu wa sekondari na msingi ni elfu 9,800 out of tunaowazalisha wenye first degree ya education ambao ni 14,664.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni ukweli kwamba bado mahitaji ya ajira na upungufu uliopo ni lazima vioanishwe ili tuone kwamba tunapunguza upungufu uliopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hili suala la ajira linakuwa kama zimamoto. Hivi kwa nini Serikali haina mpango maalum, kwamba katika mwaka mmoja wa Mwaka wa Fedha, inakuwepo kabisa, tuna mpango katika mwaka mmoja wa fedha ni lazima tuajiri kiasi fulani, inabaki ni utashi wa awamu hiyo…

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri wa nchi.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani katika hili kabla sijapata muda wa kujibu baadaye nafikiri nilitolee taarifa, kwamba Serikali haiajiri kwa utashi. Bunge lako Tukufu ndilo linalotupitishia bajeti hapa kila mwaka, na katika kila bajeti ya mwaka tumekuwa tunasema tunaajiri idadi gani ya watumishi. Bajeti ya mwaka 2021/2022 ndiyo ajira hizi ambazo tutakamilisha na nyingine 32,000 ambazo tutazitoa na tumeshazitangaza, kati ya ajira elfu 44 plus zilikuwa zote kwenye bajeti na kamati ya USEM nadhani wao wanajuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mwaka huu wa fedha unaokuja 2022/2023 tumeweka, nimesoma hapa kwenye bajeti, tumeweka bajeti ya watumishi 30,000. Kwa hiyo naomba niseme kwamba hatuajiri kwa utashi ama mtu anaamka tu, hapana. Kwa hiyo tusipotoshe. Serikali inaajiri, na kuna vigezo ambavyo vitafikia idadi hizo ambazo za watumishi tunaotakiwa kuajiri katika hilo naomba niliweke sana.

MWENYEKITI: Ahsante kwa taarifa Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Paresso unapokea taarifa.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hiyo taarifa. Hakuna ambaye hafahamu nchi hii awamu ya tano ajira zilizotolewa ni kidogo na wakati mwingine zilikuwa hazipo kabisa, huo ndio ukweli. Halafu tuliondoa watumishi hewa wengi na hatukuajiri, nani ambaye hajui? Tunamshukuru leo Rais Samia angalau hizi japo ni chache lakini zimetoka na wananchi wameziona na wamezisikia, huo ndio ukweli. Kwa hiyo taarifa siipokea ukweli utabaki hivyo kama ulivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kushauri lazima kuwepo na mpango, kwamba Serikali kila mwaka ni lazima, kwa sababu unaangalia wahitimu tunaowatoa kwenye vyuo vikuu ni wengi, hao mwisho wa siku wanaenda. Kwa hiyo tuna wahitimu tunaowatoa kuna wanaostaafu lakini hatuajiri tunasubiri tu, tunaangalia hatuna mpango hatuna utaratibu hatuna chochote tunasubiri tufanye hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilindie muda wangu mawaziri wana nafasi ya kujibu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Paresso hebu keti kwanza Mheshimiwa Naibu Waziri hebu keti kwanza. Mheshimiwa Paresso hili Bunge linakutana kila mwaka kujadili bajeti, linapitisha ndiyo hoja ya Waziri pale. Kwa hiyo unapoenda kuajiri ili uajiri lazima u-create nafasi iwepo, iwe wazi utafute bajeti utafute fedha halafu unatangaza.

Kwa hiyo, hoja aliyoitoa Mheshimiwa Waziri tulidhani pengine imeeleweka vizuri. Ninakuruhusu kuendelea kuzungumza lakini you take into consideration la sivyo nitatumia mamlaka ya kiti changu.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, no mimi hiyo taarifa siipokei na huo ndio mchango wangu na hayo ndio maoni yangu mawaziri watapata nafasi ya kuchangia katika hayo.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendele kuchangia na muda wangu ulindwe.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nollo nimekuona; taarifa.

T A A R I F A

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe tu taarifa mzungumzaji, kwamba kuajiri si kwamba ni jambo la kila wakati unalifanya unategemea na national wages. Kwa hiyo unaweza ukadhani kwamba Serikali inabana isiajiri; kuajiri inategemeana na GDP kuna percentage yake. Kwa hiyo unaweza kuona kwamba Serikali haitaki kuajiri zipo economics ambazo zinafanya kwamba na kuajiri uende kwa stahili hiyo. (Makofi)

MWENYEKITI: Endelea Mheshimiwa Paresso ukumbuke muda wako unakaribia kwisha kwa hiyo uanze ku-wind up (kelele)

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba muda wangu ulindwe.

MWENYEKITI: Unapokea taarifa?

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio hicho ninachotaka kusema kwamba hata anachoeleza Mheshimiwa Nollo haya yanayosemwa yawekwe kwenye mipango na watu wajue, kwamba wage bill ni kiasi gani according to wage bill tunaweza kuajiri kiasi gani huo ndio ukweli na ndicho ambacho tunatamani kukisikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia suala la utawala bora. Utawala bora ni pamoja na kuhakikisha sheria kanuni mifumo na taratibu inafuatwa. Katika nchi hii watanzania wengi wapo wamekuwa clustered kwenye vijiji, na katika vijiji kuna taratibu ya kuendesha mikutano mikuu ya vijiji na kufanya maamuzi ya miradi mbalimbali ya maendeleo, ya mapato na matumizi na kila kitu. Sasa, kumeibuka utamaduni, kwamba mikutano mikuu ya vijiji siku hizi haifanyiki, mikutano mikuu ya vijiji kwa mujibu ya sheria kusoma mapato na matumizi haifanyiki, mipango mbalimbali ya miradi maendeleo katika vijiji haifanyiki; sasa, huu ndio utawala bora ambao tunapaswa kuusimamia na wananchi wakaulewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nchi hii kuna baadhi ya watendaji wa kata na vijiji na wenyeviti wa vijiji, baadhi si wote, wanageuka miunguwatu kwenye maeneo yao, wananchi hawawezi kuwahoji. Baadhi ya watendaji wa vijiji leo wanafanya majukumu ya kutengezea watu tuhuma, wao ni polisi wanakamata wao ni mahakama wanahukumu, wao wanapokea faini. Yaani wao ni final kwenye vijiji na kata zao. Hii haiwezi kukubalika, huu si utawala bora. Ni lazima sasa Serikali mkomeshe huu utamaduni unaotaka kujengeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona jana kwenye mitandao ya kijamii mwananchi mmoja amekatwa panga kwa sababu alikuwa anahoji mapato na matumizi kwenye Mkutano Mkuu wa Kijiji. Sasa ni haki ya mwananchi, ni lazima hao watu wajue kwamba mabosi wao ni wananchi wa Tanzania, wanaweza wakawahoji as long I am-provoke na kwamba havunji sheria hivyo ana wajibu wa kuhoji mapato na matumizi na wale wenye mamlaka kwenye vijiji lazima wahitishe mikutano kwa mujibu wa taratibu. Tunaomba hili lisimamiwe kwa dhati kabisa ili wananchi wafurahie kuwa Watanzania. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu ya Wizara ya Afya. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu pamoja na timu yake, kwa kweli wanajitahidi na wanafanya vizuri. Pia Wizara hii imekuwa ikitupa ushirikiano sisi wajumbe wa Kamati kwa kadri inavyowezekana hongereni sana.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia katika maeneo mawili. Hoja ya kwanza ni katika eneo ya magonjwa yasiyoambukiza. Tunapoongelea afya ya Watanzania au magonjwa ambayo mengi yanayowasumbua Watanzania leo, mengi ni magonjwa yasiyoambukiza. Tafiti zinaonyesha asilimia 40 ya vifo nchini vinatokana na magonjwa yasiyoambukiza na magonjwa haya ni kansa, sukari, pressure na kadhalika. Kwa kiwango kikubwa haya magonjwa yasiyoambukiza kwa namna moja ama nyingine kama tukiwa na mikakati ya kutosha kama Serikali lakini kama jamii ikatambua athari ya magonjwa yasiyoambukiza basi tunaweza kupunguza kwa kiwango kikubwa na badala ya Serikali kufikiria kutibu, kwa sababu tunavyoongelea Hospitali za Rufaa zina upungufu wa dawa na kila kitu ni kwa sababu ya ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza. Sasa tukiweka nguvu huko maana yake tutaweka kinga zaidi badala ya kutibu.

Mheshimiwa Spika, hata leo Serikali wanapoomba bajeti kwenye Wizara hii ya Afya zote zinaenda kutibu siyo kukinga, kwa sababu ya aina ya maisha ya Watanzania ambayo tulikuwa nayo huko nyuma, tumepata magonjwa yasiyoambukizwa kwa wingi. Hivyo tunaweka nguvu kubwa katika kuyatibu. Nashauri Serikali na wadau mbalimbali sasa tuweke pia nguvu kuhakikisha tunaweka kinga kwa magonjwa yasiyoambukiza ili hii asilimia 40 ya vifo inayotokana na magonjwa ya kuambukiza, basi tuweze kuipunguza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo lazima jamii ipewe elimu na kueleweshwa. Kuna mambo mengine kwa mfano mtindo wa maisha tunayoishi, wakati mwingine yanapelekea ndiyo tunapata sukari, tunapata pressure, mtu anaona anaishi maisha fulani ndiyo yuko sawasawa kumbe siyo sahihi. Kwa hiyo nadhani Serikali kwa kushirikiana na Wizara nyingine mtambuka pamoja na wadau tuone namna ya kubadilisha maisha ya Watanzania tunayoishi.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano, leo vijana wetu wa bodaboda wanaendesha bodaboda siku nzima, ok wamejiajiri wapate kipato lakini hawa vijana wanakunywa kinywaji maarufu kinachoitwa energy drink ambazo ziko za aina mbalimbali. Hawa vijana wanaweza kunywa energy drink tatu, nne, tano kwa siku, huyo utegemee baada ya miaka 10 au 20 Serikali tutaanza kumtibu kwa sababu amepata magonjwa yasiyoambukiza. Yeye leo anaona yuko sawasawa inawezekana hajui madhara na ni kweli kwamba wengi hawajui madhara.

Mheshimiwa Spika, siyo hao tu nimetoa mfano mmoja wa kundi moja la vijana wa bodaboda kwa sababu tunawaona, wako wengine wengi tu wa makundi mbalimbali hata watu ambao wapo maofisini, kwenye sekta binafsi mtu anaona kunywa energy drink labda ni Red Bull au nini ananunua 3,000 mpaka 4,000 anaona ni ufahari kwa sababu ni kinywaji ambacho angalau kina bei fulani, kumbe ni kinywaji ambacho tunajitengenezea matatizo mwisho wa siku tunapata kansa, tunapata kisukari, sijui wanasema maini yanavimba, mimi sielewi vizuri utaalam. Lakini yote hayo yanapelekea kwenye…

SPIKA: Mheshimiwa Cecilia Paresso ngoja, ngoja twende vizuri kwa sababu hapa Bungeni pamoja na mambo mengine hizo biashara zinazosemwa hapo ni biashara za watu, sijajua kitaalam kama hivyo vinywaji unavyovisema ndivyo vinavyoleta hayo magonjwa unayoyasema. Maana kama Serikali imeruhusu viuzwe halafu vina madhara hayo makubwa unayoyasema itakuwa mtihani. Hapa kuna kimoja ambacho umekitaja mahsusi. Sasa ili usitupeleke kwenye hiyo hoja, hoja yako ni ya msingi lakini usitupeleke kwenye hiyo hoja ya wafanyabiashara fulani kuona wao wanaonewa na Bunge. Hebu hiyo sehemu ya mchango wako rekebisha.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa maelekezo. Nirekebishe tu kwa kusema vinywaji vya kuongeza nguvu kwa ujumla wake vinavyoitwa energy drink kwa ujumla wake, sasa pamoja na kwamba vinapata kibali vinaingizwa, lakini Serikali ione namna gani ya kutoa maelekezo ya unywaji ulio bora ili tusije tukaingiza Taifa au watu wetu kwenye magonjwa yasiyoambukizwa kwa kuleta madhara kimwili na kiafya. Kwa hiyo hilo ni upande mmoja katika vinywaji hivi vya kuongeza nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna suala la utumiaji usio sahihi wa…

SPIKA: Sasa Mheshimiwa Paresso hapo umeeleza vizuri, hebu sasa ondoa yale maneno yako ya Red Bull.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naondoa yale maneno niliyotaja ya Red Bull.

Mheshimiwa Spika, suala lingine pia ni utumiaji usiyo sahihi wa viatilifu kwa wakulima. Wakulima wetu wengi wanatumia hayo madawa mashambani kwa namna isiyo sahihi, pamoja na kwamba vinapata vibali, vinaingia, kuna ukaguzi na vitu kama hivyo, lakini hawatumii kwa namna isiyo bora. Kwa hiyo wasipotumia kwa namna isiyo bora tutegemee mwisho wa siku na huko vijijini tunaona. Kwa mfano sisi tunaotoka Karatu kuna bonde moja linalima vitunguu pale.

Mheshimiwa Spika, ukifika wakati wa kupulizia dawa wanapulizia tu ilimradi mtu anachukua bomba anapuliza, hana namna yoyote ya kujikinga. Kule pia kuna shida kubwa watu wanaanza kuwashwa na wanaanza kupata magonjwa ya ngozi. Huyu mwisho wa siku akiendelea muda mrefu kuna nafasi kubwa sana ya kupata ugonjwa wa kansa. Kwa hiyo iko namna ya kutazama pia kwa wakulima wetu tuwasaidie, kuwepo na mbinu mbadala kwa kushirikiana Wizara husika na Wizara zingine Wizara za Kisekta tuone namna gani pia wakulima wetu watumie kwa usahihi hivi viatilifu ili kuondokana na hatari ya kuingia kwenye magonjwa yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Spika, kuna suala lingine pia, suala la kutokufanya mazoezi ni sehemu pia ya namna ambavyo tunajiweka kwenye mazingira hatarishi ya kupata magonjwa yasiyoambukiza. Tunafahamu siku hizi kuna kampeni mbalimbali za kufanya mazoezi, ni kweli lakini ni wachache, Watanzania walio wengi bado hawajui manufaa ya kufanya mazoezi. Mfano mtu anakaa ofisini au yuko nyumbani anafanya hivi, anakula wanga wa kutosha akitoka hapo hafanyi mazoezi hajishuhgulishi hafanyi chochote. Huyu utegemee baada ya miaka 10, 20 anaanza sukari, anaanza pressure, Serikali inaanza kuweka nguvu kubwa sasa ya kutibu pressure yake na sukari yake, lakini kumbe tungeweza kuweka nguvu kubwa ya kupunguza hiyo life style yake au kwa kufanya mazoezi kwa kupunguza hatari kubwa ambayo iko mbele yake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitoe rai kwa Serikali pamoja na wadau tuweke nguvu kubwa ya kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza, tutoe elimu kwa Watanzania kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, Watanzania wajue namna ya ulaji sahihi na kwa wakati, wafanye mazoezi, ili basi tuone kwamba tunapunguza haya yaliyoko mbele yetu ya vifo karibu asilimia 40 vinavyotokana na magonjwa yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Spika, suala la pili nizungumzie vifo vinavyotoka na uzazi. Kupitia Hotuba ya Waziri ameeleza vizuri sana angalau vinapungua vifo hivi vinavyotokana na uzazi, lakini bado takwimu zinaonyesha vifo hivi bado ni vingi sana. Pamoja na kwamba kuna jitihada zinazoendelea lakini pia uhudhuriaji wa clinic kwa akinamama wajawazito umeeleza na mpango wa kuhakikisha Serikali inatoa elimu kwa akinamama wanaohudhuria clinic ni jambo moja zuri, lakini hata pale wanapofika clinic wanapokelewaje, hapo pia kuna tatizo kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, mtu anaweza akaenda tu anapimwa anaondoka zake, yaani samahani kusema haya, baadhi ya manesi utakuta tu maskini anampokea mama mjawazito yeye mwenyewe amenuna kweli kweli. Yaani huwezi jua alikotoka kule ana mazingira gani, inawezekana ugumu wa maisha, inawezekana ndivyo alivyo, lakini tuangalie pia hii customer care kwa akinamama wanaofika pale clinic, anapokelewaje. Ndiyo atahudhuria, tutawahamasisha kweli wahudhurie na hapa wameonyesha takwimu zinaongezeka kidogo, lakini bado wako wengine wengi ambao hawahudhurii. Akifika pale anapokelewaje, anakaguliwaje, yuko katika hatua gani anapewa maelekezo gani na maelekezo gani na maangalizo gani ili anapofikia hatua za kujifungua au akiona dalili fulani hatarishi afanye nini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hilo ni muhimu sana, wakaweka ama ni dawati hapo pekee maalum, akishamaliza kwenye vipimo awe na mtu wa kumsemesha. Nikwambie ugumu wa maisha uliyopo leo pia kwa kiasi kikubwa unachangia, mama ametoka huko maskini ana stress za maisha huko, stress za familia, jamii inayomzunguka akifika pale anatamani apate comfort fulani kwa kuongea unajua sijui wataalam wanasema hata ukisema una-release stress uliyonayo. Kwa hiyo afike pale kwenye kituo anaenda clinic lakini anakutana na mtu ambaye pamoja na atampa ushauri wa hali yake ya ujauzito lakini apate hata haya mengine ya kupumua ili huyu mama mwisho wa siku aweze kujifungua salama.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, mchango wangu ni huo. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu kuhusu hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyoiwasilisha hapa Bungeni. Nianze kwa maneno ya utangulizi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba nchi yetu imejaliwa au imebarikiwa rasilimali nyingi na za kutosha na tuna utajiri wa kutosha sana. Imekuwa tu ni bahati mbaya rasilimali na utajiri tulionao unatumika vibaya na unatumika kwa wachache na walio wengi hawanufaiki na rasilimali. Ni vema tukatambua na tukakumbushana kwamba hii Nchi ni ya Watanzania wote, hii nchi sio ya watu wachache. Vile vile ukitaka kujua jinsi gani nchi hii inaliwa, ripoti ya CAG imeonesha ubadhirifu mkubwa, matumizi makubwa na mabovu ya rasilimali fedha za Watanzania na ufisadi, upigaji wa dili na kila kitu umeoneshwa katika ripoti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukitaka kumsaidia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ni lazima kwa wale wote ambao wamehusika kwa namna moja ama nyingine tuone neno uwajibikaji kwa vitendo. Bahati mbaya sana neno uwajibikaji halijawahi kutokea ila tumezoea mpaka tuone tumetenguliwa, tumepangiwa kazi nyingine, tumeondolewa lakini haijawahi kama ni mtumishi kama ni kiongozi akawajibika. Kama tunampenda Mama Samia waliohusika kwa namna moja ama nyingine wawajibike katika nafasi zao. Vile vile tunataka rasilimali za Watanzania, fedha za Watanzania ziwafaidishe Watanzania wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweza ukashangaa na kujiuliza…

MHE. CATHELINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. CATHELINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuzingatie kanuni, muda wa kujadili taarifa ya CAG bado haujafika.

NAIBU SPIKA: Huo ndio ukweli lakini, kwa sababu CAG ame-cite mapungufu aliyoyaona yeye, yanakuja Bungeni, sasa Bunge ndilo lenye kuamua baada ya kuhoji pande zote. Kila Mtu ana haki ya kusikilizwa, sasa kama mnafurahi tu kwenda kuwachanganya wananchi, hii sio sahihi. (Makofi)

Endelea na mchango wako.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Sasa bahati mbaya sana pia badala ya kuisaidia nchi hii tukiwa tunajificha kwenye taratibu na nini nadhani sio sahihi. Ndio maana kama tungekuwa tunataka kweli kumsaidia Rais hata haya mambo tungeyajadili kwa dharura. Ni kiasi kikubwa cha fedha kimeonesha ubadhirifu mkubwa. Anyway, utaratibu upo lakini mwisho wa siku ni lazima tutafakari na kufanya maamuzi kwa maslahi mapana ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nifanye reference hapa kwa sababu kufanya reference haikatazwi na ikishaletwa hapa, maana yake it is a public document na ipo kwenye mitandao na iko kila mahali. Saa unaweza ukajiuliza, tunatumia fedha nyingi kuhifadhi vyura Marekani badala ya kumhudumia Mama wa Kitanzania ambaye anaenda kujifungua leo. Inasikitisha yaani nini kipaumbele chetu cha kwanza kwa Mtanzania? Kwa hiyo ni mambo kama haya na mengine mengi sasa wakati ukifika tutajadili kwa undani zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, huo ulikuwa ni utangulizi, sasa nijikite kuchangia kwenye Sekta ya Ardhi. Ardhi ni mtaji, ardhi ni rasilimali muhimu sana na tuna bahati kama nchi tuna ardhi ya kutosha na nzuri ambayo inafaa kwa matumizi mazuri. Ardhi yetu ni lazima ipangwe, ipimwe na kumilikishwa na lazima tutambue kwamba ardhi haiongezeki lakini mahitaji ya ardhi yanaongezeka na watu ambao wanahitaji ardhi wanaongezeka. Sasa ni lazima Serikali iweke mipango mizuri ya kuhakikisha masuala ya upangaji wa ardhi, umilikishaji wa ardhi na matumizi ya ardhi kwa ujumla yanafanyika kwa wakati na yanatiliwa msisitizo wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hali iliyoko sasa hairidhishi na haiendani na uhitaji na bahati mbaya sana takwimu zinaonesha toka tumepata uhuru kati ya vijiji 12,319 ni vijiji 2,600 tu ndivyo ambavyo vimepimwa kwa matumizi bora ya ardhi, toka tumepata uhuru mpaka leo tunapoongea. Sasa ni vizuri sana tukaweka fedha za kutosha kuhakikisha kama tunaweka mkazo wa kupima ardhi yetu ya vijiji tunavipima kweli kweli, kama tunapima kwenye haya maeneo mengine, tunapima. Kwa hiyo, kwa kufanya hivyo maana yake tutapunguza kwa kiwango kikubwa migogoro ya ardhi. Kwa hiyo, tujikite katika kupanga matumizi bora ya ardhi, tusijikite katika kutatua migogoro, tukipanga tutapunguza migogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaona Kamati ya Mawaziri inazunguka nchi nzima, ile ni gharama, wanatumia fedha, wanatumia gharama kubwa, lakini kama tungewekeza katika kupanga tungepunguza haya mengine ambayo yanajitokeza leo. Kama haitoshi kati ya mwaka 2013 mpaka mwaka 2022, Serikali ilipanga kurasimisha maeneo 2,348,000 ili wapatiwe hati, lakini mpaka leo mwaka 2022 ni takribani miaka nane, ni maeneo 171,210 ndio peke yake yamerasimishwa na yakapewa hati. Miaka 8 tumeweza kurasimisha kwa asilimia saba tu. Sasa tutegemee ni kwa kiwango gani tutafikia kurasimisha kwa kiwango kikubwa ardhi yetu? Ardhi yetu ndiyo mtaji wetu, ardhi yetu ndiyo rasilimali yetu Watanzania. Kwa hiyo, ni lazima pawepo na msisitizo wa kuhakikisha ardhi hii ya Watanzania inapimwa kwa kadri ya mahitaji na kulingana na soko lilivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama haitoshi mwaka 2012, Serikali ilitarajia kutoa hati miliki 1,638,000, lakini kwa mwaka huo tu waliweza kufanikiwa kutoa hati 643,000. Sasa kama nilivyoeleza kwa kutumia ardhi hii tu Serikali ingeweza kupata mapato ya kutosha sana. Kwa hizi hati ambazo zimetolewa 643,000 ukichukua kiwango cha juu kabisa ukasema kila mwenye hati alipe angalau Sh.120,000 ya kodi kwa mwaka, maana yake Serikali ingepata mapato ya Shilingi Bilioni 77.2 kwa hati hizo chache tu. Vipi kama tukiweza kupima ardhi nzima ya Tanzania tukatoa hati, wenye hati wakailipa kodi kwa wakati? Kwa hakika Serikali ingeweza kupata mapato ya kutosha na yale mahitaji ya msingi ya Watanzania yangeweza kuwafikia kwa wakati na lakini kuhakikisha tunadhibiti ufisadi na mianya yote ya upigaji. Maana yake tungeweza kutengeneza namna bora ya kupata mapato halafu tukatengeneza na namna nyingine ya kupiga mapato haya bila kuwafikia watanzania kwa ujumla. Kwa hiyo haya ni muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kama haitoshi, kuna maeneo makubwa ambayo yanaitwa kwa majina tofauti tofauti. Mfano sisi kule Kaskazini, tunaita mashamba makubwa ya Wawekezaji, kuna mashamba ya settlers, maeneo mbalimbali nchi nzima. Hao wamekuwa wakimiliki ardhi kwa muda mrefu wana lease ya miaka 99, wengine wamelimiliki toka wakati wa ukoloni mpaka leo, lakini wapo wengine ambao wanabadilisha matumizi ya ardhi hii bila kufuata utaratibu. Wako wengine ambao wametekeleza mashamba haya, wako wengine yaani inakuwa ni marufuku kuingia kwenye haya mashamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano maeneo ya kaskazini, maeneo ya Meru kule, Maeneo ya Karatu, haya mashamba wanaomiliki wameacha mapori, wanyama wanajihifadhi humo, wananchi wanateseka katika nchi yao wakiwa wanaenda, mfano mmoja, kwenye shamba mojawapo katika Wilaya ya Karatu, mwekezaji ameacha pori, hilo pori wananchi wanapita kwenda kupeleka watoto shuleni. Juzi kati hapa mama ameuawa na mbogo akiwa anampeleka mtoto shuleni asubuhi, lakini eneo limeachwa ni pori linahifadhi. Halmashauri haiwezi kufanya kitu, Mwekezaji anasema ni mali yake ndiye ameamua hivyo kwa sababu ana hati. Haiwezekani lazima ifike mahali tuwaonee huruma Watanzania, lazima ifike mahali haya mashamba ambayo kwa namna moja ama nyingine hayajaendelezwa yafutiwe umiliki Watanzania wagawiwe ardhi hii waweze kuyaendeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema watu wanaongezeka, mahitaji yanaongezeka, ardhi ni ile ile haiongezeki. Kwa hiyo, tuweke msisitizo katika kupima, kupanga na hatimaye kumilikisha kwa maslahi mapana ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ya mwisho, suala la utawala bora. Suala la utawala bora hasa kwenye halmashauri zetu na kwenye wilaya zetu kuna changamoto kubwa…

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa tungepunguza mazungumzo, tupunguze mazungumzo.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, tunategemea kuona utawala bora ni utawala unaofuata sheria, lakini kwenye maeneo yetu, utaratibu na jinsi ambavyo sheria na kanuni inataka, ni kuwepo na Mikutano Mikuu ya vijiji, kuwepo na usomaji wa taarifa ya mapato na matumizi, huo utamaduni uliishakufa na uliishapotea hakuna. Baadhi ya Wenyeviti wa Vijiji, Watendaji wetu wa Kata na Watendaji wetu wa Vijiji kule wamekuwa Miungu watu, yaani wao ndio wanafanya kila kitu, wao ndio watatengeneza michango, watakusanya wao, watapangia matumizi wao, watawatoza faini wananchi, watawaweka kwenye lockup zao wanazozijua. Hatuwezi kuwa na nchi ya namna hii…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: kengele ya pili.

MHE. CECILIA D. PARESSO: …tunataka utawala wa Sheria na utawala bora ufuatwe…

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili, ahsante.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Mchango wangu wa kwanza utajikita katika suala zima la misitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeendelea kushuhudia misitu yetu ikizidi kutoweka kwa kasi kubwa sana na hatujaona mikakati ya dhati ya Serikali kuhakikisha kunakuwa na misitu endelevu. Kuna takwimu ambazo zinaonesha national annual deforestation ni kati ya 0.8% mpaka 1.1%. Kwa kiwango kikubwa misitu hii inatoweka kwa shughuli mbalimbali ikiwemo shughuli za kilimo, uvunaji wa miti, moto na pia biashara kubwa ya mkaa. Ni vizuri Serikali ikatambua misitu hii leo tunaipoteza miaka 20, 30 ijayo nchi hii inaenda kuwa jangwa na hatujaona mkakati wa dhati kabisa wa Serikali kuhakikisha tunakuwa na misitu endelevu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba tuna hiyo TFS ambapo jukumu lake kubwa ni kuhakikisha inasimamia na kutunza hiyo misitu ya asili. Hata hivyo, hii TFS imejikita katika kukusanya mapato zaidi bila kuwa na mipango endelevu ya misitu hii. Mheshimiwa Mbunge mmoja jana alichangia hapa akahoji hata mapato yenyewe yanakusanywaje na haya mapato yanayokusanywa kweli yana uhalisia? Ukichukua mfano, kuna tafiti zimefanywa, kwa Mkoa wa Tabora peke yake kwa mwaka wanazalisha magunia ya mkaa 2,244,050 wanapata shilingi bilioni karibu 21 kwa mwaka kwa shughuli za mkaa peke yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma taarifa za TFS wao wanasema makusanyo ya mkaa tu kwa mwaka ni shilingi bilioni saba, lakini Mkoa tu wa Tabora ni bilioni 21, kitaifa wanasema ni shilingi bilioni saba. Kwa hiyo, nadhani Mheshimiwa Waziri anapaswa ku-deal na hawa watu wa TFS, kuna tatizo hapa. Kuna watafiti wamefanya utafiti wanaonesha hizi takwimu mkoa mmoja wanaingiza fedha nyingi, lakini Kitaifa TFS wanasema ni shilingi bilioni saba tu. Wizara inatakiwa kuhakikisha wanaitazama vizuri hiyo TFS kwa sababu wao nadhani ama ni rushwa ama kuna watendaji ambao si sahihi wanakwamisha shughuli hizi za kukusanya mapato. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niishauri Serikali kwamba pia wasiitazame TFS katika kuhakikisha inawaletea mapato tu au kutoa vibali vya misitu na vitu kama hivyo. Ni muhimu TFS ikatekeleza majukumu yake kama dhamira ya uanzishwaji wa TFS ilivyokuwa katika taratibu zake za uanzishwaji. Ni muhimu sana Serikali mkatazama hawa TFS wanapotoa leseni, watoe leseni lakini hao wanaopewa leseni walete mpango mbadala au mkakati mbadala wa kuendeleza misitu yetu ili tuweze kuondokana na kutoweka kwa misitu kwa kiwango kikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la migogoro ya mifugo inayoingia hifadhini. Waheshimiwa Wabunge sisi kama viongozi pia wakati mwingine ni lazima tuangalie kauli zetu zisije zikalibomoa Taifa. Ni kweli kwamba tunawahitaji wafugaji, ni kweli tunawahitaji wakulima, ni kweli kwamba tunahitaji hifadhi au misitu. Ni muhimu tukafahamu kuwa mifugo inaongezeka na mahitaji ya kilimo kwa maana ya wakulima wanaendelea kuhitaji ardhi lakini ardhi ni ile ile tu haiongezeki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri sana Serikali wakakaa na Wizara zote ambazo zinaingiliana katika masuala haya ya mifugo, kilimo na wa maliasili kuhakikisha wanaweka mipango madhubuti ya kuhakikisha wafugaji wanapata maeneo yao, wanatengewa kabisa, hifadhi nayo inakuwa na maeneo yasiingiliwe na wafugaji, vivyo hivyo kwa wakulima pia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kusema pia wakati mwingine unaruhusu moja kwa moja mifugo inaingia hifadhini lakini kama hawa watu wangetengewa maeneo yao hakika tusingekuwa na hii migogoro ambayo inaendelea. Serikali lazima ipime, ukipima kati ya suala la maliasili na utalii na kati ya sekta ya mifugo utaona kwa takwimu kwa sasa kwamba maliasili inaiingizia Serikali pato zaidi kuliko mifugo. Inawezekana pia mifugo ingeweza kuliingizia Taifa pato zaidi kuliko maliasili lakini kama wangekuwa na ufugaji wa kisasa, wakapangiwa maeneo yao, wasiingiliane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni muhimu sana Serikali wakayapima haya, wakahakikisha migogoro hii ya wakulima na wafugaji inakwisha. Niwasihi Waheshimiwa viongozi wenzangu Wabunge, ni muhimu sana tukachunga kauli zetu, tuangalie tunawahitaji watu wote. Tunawahitaji wakulima, tunawahitaji wafugaji, tunahitaji pia na misitu yetu na uhifadhi kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la utalii. Wizara imetoa takwimu hapa kwamba kwa mwaka nchi yetu inaingiza watalii karibu 1,200,000 na kuna Mheshimiwa Mbunge wa Arusha jana alichangia vizuri sana akafanya comparison na nchi nyingine ambazo zinakuwa na idadi kubwa ya watalii. Nchi yetu mtalii kuja hapa anakumbana na tozo kibao. Anaanzia kwanza kwenye viza, akienda kama ni Ngorongoro getini kuna fees, akilala kwenye hoteli kitanda kina fees, kila mahali Mzungu huyu au mtani huyu anatozwa tozo na hizi tozo zimekuwa ni fixed mwaka mzima na watalii ni wale wale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niishauri Serikali kwa nini msiwe na promotion package kwa kipindi fulani ili muongeze idadi ya watalii halafu baadaye mkifika kwenye pick fulani mtaendelea na hizi tozo zenu ambazo ziko fixed ili tuhakikishe tunaongeza idadi ya watalii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ni muhimu sana pia wakahakikisha wanakuza utalii wa ndani. Kuna baadhi ya maeneo, mimi natoka Wilaya ya Karatu, Wilaya ya Karatu ina hoteli za kitalii 54, wako Watanzania ambao hawajui. Mtanzania yuko Dar es Salaam anafikiria kwenda kupumzika South Africa lakini kumbe angekuja kupumzika Karatu kuna hoteli nzuri, zile ambazo wanazifuata nje ya nchi pia ziko pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti,una hoteli nzuri sana ambazo wageni wengi wanapenda kulala pale halafu wanakwenda kutembea Ngorongoro. Wilaya kama hizi ambazo ziko pembezoni mwa Hifadhi ya Ngorongoro ambayo ni sehemu ya lango la kuingilia Ngorongoro tayari kuna hizi hoteli za wawekezaji na wazawa pia wamejitahidi kujenga hoteli za standard mbalimbali, unakuta kuna hoteli ya mpaka kulala siku moja ni karibu dola 700, hoteli yenye standard na quality ya juu kuliko labda hizo mnazofuata South Africa na kwingine, ziko Karatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni muhimu pia Wizara wakaangalia Wilaya kama hizi ambazo tayari kuna hoteli kama hizi wakazitangaza, wakafanya utalii wa ndani pia wakawa na target ya kukuza utalii wa ndani na si tu kuangalia target ya kukuza utalii wa wageni kutoka nje. Kwa hiyo, ni muhimu sana wakalitazama hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu TANAPA. TANAPA ina jukumu la msingi la kusimamia hifadhi za Taifa, uhifadhi wa wanyamapori na shughuli za utalii. Leo TANAPA mapato yake yote yanapelekwa kwenya pool moja kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali, lakini hawa baadaye wakitaka kutekeleza shughuli zao maana yake waje tena waombe huko, kwa maana ya Hazina au Mfuko Mkuu wa Serikali waweze kwenda kutekeleza majukumu yale. Mfano, leo pale Ziwa Manyara liko chini ya hifadhi ya TANAPA linapotea kwa sababu limejaa tope hakuna kinachofanyika. TANAPA wanakusanya fedha badala nyingine zirudi kwenda kutekeleza zile shughuli zinapelekwa Mfuko Mkuu wa Hazina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wanaipa TANAPA kazi ya kutengeneza madawati nchi nzima halafu Waheshimiwa Wabunge wanapongeza wakati TANAPA ina kazi ya kudhibiti ujangili, ina kazi ya kudhibiti na kuhakikisha kunakuwa na uhifadhi endelevu, ina kazi ya kuhakikisha mfano Ziwa Manyara linaendelea kuwepo? Mheshimiwa Waziri baada ya miaka 10 au 20 Ziwa Manyara linapotea kwa sababu limejaa tope maji yale yanakuwepo tu msimu wa masika baada ya muda ni tope linajaa pale. Kwa hiyo, ni muhimu sana Wizara wakaangalia shughuli za TANAPA zisiweze kusimama. Haiwezekani wao wanakusanya fedha wanawapelekea halafu mwisho wa siku yale majukumu yao ambayo wanapaswa kuyafanya hawawezi kuyatekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuongelea kuhusu Operesheni Tokomeza. Kwa kuwa kulikuwa na Azimio la Bunge kwa wananchi walioathirika na Operesheni Tokomeza ni muhimu sana Serikali ikahakikisha inalipa fidia kwa wakati kwa wananchi hao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ni kuhusu leseni ya biashara ya Nyara, kuna baadhi ya kampuni zilizopewa leseni hizo na baada ya muda leseni zikafutwa na tayari kampuni hizo zilishakuwa na nyara hizo na baada ya muda wahusika kukamatwa ilhali wakati wanatekeleza jukumu hilo walikuwa na leseni halali. Serikali itueleze kwa nini kumekuwa na mkanganyiko huu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, Wilaya ya Karatu inapakana na TANAPA (upande mmoja) na Hifadhi ya Ngorongoro (kwa upande mwingine). Wilaya imekuwa haina makubaliano ya kimkataba wa namna gani Wilaya hiyo inafaidika na utalii ili kujenga ujirani mwema. Misaada hiyo imekuwa inatolewa bila ya kuwa na uhakika wa kuipata (hisani). Ni kwa nini mamlaka hizi zisiingie makubaliano rasmi ya kimkataba ili Halmashauri iwe na uhakika kwa mwaka ni miradi ipi, kwa gharama ipi itatekelezwa na mamlaka hizo? Ni muhimu mambo haya yakawekwa wazi ili kujenga ujirani mwema.
Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika hizi taarifa zilizowasilishwa mbele yetu, taarifa ya Kamati ya PAC na LAAC. Mchango wangu wa kwanza utajielekeza katika suala zima la Deni la Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi Juni, 2016 Deni la Taifa limeongezeka kwa asilimia 9.76 maana yake linakimbilia shilingi trilioni 40. Madeni haya kwa mujibu wa taarifa ya CAG ameeleza kabisa hakuna mkakati wa namna gani yanaweza kwenda kulipika. Kulikuwa kuna rasimu ya mkakati huu ya mwaka 2002, ikatengenezwa rasimu nyingine ya mwaka 2004, ikatengenezwa nyingine ya 2014 lakini zote ni rasimu bado haijakamilika kuwa mkakati wa kuona namna tuta-control Deni la Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tusipoangalia, itafikia mahali fedha zote za makusanyo ya nchi hii zinaenda kulipa madeni. Kama ambavyo ilivyo leo kila kinachokusanywa karibu shilingi bilioni 900 inaenda kulipa madeni. Kwa hiyo, ni lazima Serikali ifike mahali iandee mkakati. Ripoti ya CAG imesema kabisa hii rasimu ambayo ipo tena imeandaliwa kizamani haiendani na hali halisi ya uchumi wa nchi. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikaona umuhimu wa kuwa na mkakati huu ambao utaendana na hali halisi ya uchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee kuhusu Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Tuna Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambayo kwa kiwango kikubwa fedha zake zinakopwa na zinaenda kuwekezwa katika miradi mikubwa. Hatukatai kufanyia shughuli hizo, lakini unapoenda kukopa halafu hurejeshi inakuwa ni tatizo. Mfuko mmojawapo tu kwa mujibu wa taarifa ya CAG ni PSPF una hali mbaya ambapo unakaribia kufilisika kabisa kwa sababu Serikali hairejeshi fedha ilizozikopa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni lazima ifike mahali muache kabisa kukopa hizi fedha za wanachama. Ni fedha za wanachama wanaweka kule wakijua wanajiwekea akiba lakini Serikali mnaenda kuzichukua na ku-invest kwenye miradi mikubwa ambayo tunaona kabisa siyo rahisi muweze kurudisha kwa sababu mmejaa madeni, mnadaiwa ndani na nje, mnakopa tena kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, mnadaiwa kila kona, mwisho wa siku mtaenda kuua hii akiba ya wafanyakazi ambao wanatarajia waipate siku wakistaafu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshaongelea sana suala la kuunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, tumesema sana kwenye Bunge la Kumi. Leo mnajiita wazee wa hapa kazi tu, wazee wa kubana matumizi, si ndivyo mnavyojiita? Kama kweli mnataka kubana matumizi ni lazima muangalie suala la kuunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Hii Mifuko ya Hifadhi ya Jamii iko takribani tano au sita yote ina Wakurugenzi, ofisi, inaendeshwa kwa gharama na kwa fedha za wanachama. Kama mnasema mnabana matumizi muende muunganishe hii Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kuwepo na ama mifuko miwili au mitatu ili hicho mnachokiita cha kubana matumizi mkifanye kwa vitendo siyo mnatuambia tu halafu hakuna mnachokifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya mwisho nitajielekeza katika Serikali za Mitaa. Katika Awamu hii ya Tano mnaenda kuua kabisa Serikali za Mitaa. Mnaenda kuzimaliza wakati Serikali za Mitaa zipo kwa mjibu wa Katiba ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza uteuzi tu mliofanya, Mheshimiwa Rais alifanya uteuzi wa hawa ma-DC, ma-DED, ma-DAS, kwa kweli ni watu ambao hawajapitia kwenye mifumo ya local government, wengine wametolewa mnakojua, wamepewa nafasi ambazo hawana experience hata nukta moja. Hivi wanaendaje kufanya kazi? Ma-DED wengine hawajui hata vote ni nini, anauliza vote ni nini? Wanauliza hawajui. Hivi mnategemea kutakuwa na ufanisi? Ndiyo maana tunawaambia mnaenda kuua Serikali za Mitaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali miaka yote imeonesha suala la Serikali Kuu kutokupeleka fedha za maendeleo katika Halmashauri za Wilaya. Hivi tunavyoongea leo, fedha zilizoenda katika local government ni fedha za mishahara tu. Mfano mzuri ni Halmashauri yangu ya Karatu. Fedha kidogo tu iliyoenda ni ya barabara shilingi milioni 50 lakini hakuna fedha za miradi ya maendeleo zilizoenda yaani mpaka leo tunaingia robo ya pili ya bajeti ya Serikali fedha hazijaenda katika Serikali za Mitaa. Mnatarajia nini si mnaenda kuziua Serikali za Mitaa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Hoja ya Wizara ya Maliasili. Kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri kwa kuteuliwa kuongoza wizara hiyo ni miongoni mwa Wizara ambazo tuseme ni ngumu au zina changamoto nyingi. Historia inaonesha Wizara hii haijawahi kuwaacha Mawaziri salama huwa hawamalizi muda wao, huo ndio ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi tunakutakia kheri na tumeona jinsi ambavyyo umefanya kwenye Wizara ya Utamaduni, sasa uko Wizara ya Maliasili, jitahidi tu utulie, uielewe vizuri wizara na sekta zake zote, upate ufahamu ufanye engagement na wadau mbalimbali, usikilize maoni ya wananchi, usikilize maoni ya Wabunge, utatue changamoto za muda mrefu na utafanikiwa na unaweza ukadumu hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo nianze pia kwa kutoa pole kwa familia ya baba mmoja wa familia ambaye ameuwawa leo asubuhi na tembo akiwa shambani kwake katika Kata ya Oldeani, Wilaya ya Karatu, Mungu amlaze mahali pema peponi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia hoja yangu ya kwanza migogoro mingi ambayo tunaiona kati ya hifadhi na wananchi na yote ambayo yanaendelea kwa namna moja ama nyingine, migogoro hii ni ya siku nyingi baadhi ya maeneo ni migogoro ambayo imechukua muda mrefu. Ni migogoro ambayo ukimuuliza leo mwananchi wa kawaida ambaye yupo kwenye haya maeneo ambayo yanazunguka hifadhi, kwanza mwananchi huyo haioni umuhimu wa hifadhi wala haitamani kwa sababu anapambana na hiyo changamoto ya muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimwambia mwananchi kwamba sekta hii ni sekta muhimu kwa uchumi wa nchi, ni sekta muhimu kwa kuliingizia nchi fedha za kigeni hawezi kukuelewa. Kwa sababu wameshakumbana na changamoto ya muda mrefu ambayo haitatuliki. Kwa hiyo, tunahitaji Mheshimiwa Waziri, unahitajika kwanza kurudisha imani kwa wananchi wote ambao wamekumbwa na hizi changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kujenga mahusiano mazuri, kumfanya mwananchi aone umuhimu wa hifadhi katika eneo lake yaani aone umuhimu na kutambua. Sasa wataweza kuona na kutambua kama atasikilizwa na baadhi ya changamoto ambazo amekumbana nazo za muda mrefu ziweze kuondoka na hatimaye kwisha kabisa. Naamini inawezekana, hasa migogoro hii ukisikiliza wataalamu wanasema kabisa migogoro hii ni kwa sababu kuna wananchi wamevamia shoroba, kuna wananchi wameingia kwenye maeneo ya hifadhi, kuna mifugo inaingizwa hifadhini na mambo wakadha wa kadha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najiuliza mfano swali moja ni kwa namna gani kwanza tumetambua shoroba zote? Hivi kuna takwimu sahihi ya kutambua shoroba zote ndani ya nchi hii? Halafu kuziainisha kwa kuweka labda category A, B, C zipi ambazo zimevamiwa kabisa kiasi kwamba hakuna namna inabidi tuziachie au zipi ambazo sasa zimevamiwa kwa kiasi kidogo zinaweza zikanusurika kwa kufanya maamuzi magumu ku-compensate na kuondoa wale wananchi na kuwapelekea maeneo mengine ili kuhakikisha shoroba zinaweza kendelea kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mambo ambayo yanatakiwa yafanyike kwa utulivu kwa usahihi na kufanya maamuzi magumu kwa kuwekeza fedha kama kweli tunataka kuona migogoro hii ina pungua lakini kuimarisha hizo shoroba. Ni kwa sababu tunahitaji hifadhi, tunahitaji wananchi wetu tunawahitaji, tunahitaji mambo yote. Tunahitaji hifadhi na sekta kwa ujumla isaidie katika uchumi wa nchi lakini haya yote tutakapoyahitaji maana yake lazima tufanye balancing ya mambo yote haya kwa pamoja lakini kingine kinachokosekana, unakuta kwenye eneo la shoroba kumejengwa mpaka ofisi hata za Serikali. Tunaambiwa hapo Mvomero, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya imejengwa kwenye shoroba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unajiuliza hivi mpaka inajengwa inatengenezwa plan mpaka inajengwa kumbe imejengwa kwenye shoroba. Tafsiri yake ni kwamba ama hakuna proper coordination sahihi ama utaratibu wa kupanga ardhi yetu haukamiliki au haufanyiki kwa wakati ama kuna uzembe na vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naamini kati ya kazi kubwa ambayo itakiwa kufanywa sasa ushirikiane na sekta zingine zinazohusika kwa maana ya Wizara zingine. Mfanye matumizi bora na kuzitambua haya yanayoenekana leo yasijirudie. Yaani tujue na kuzitambue kwamba hapa ni shoroba, hapa panatakiwa kujengwa hapa hapatakiwi hapa ni hifadhi hapa ni mpaka na kila kitu ndipo ambavyo tutaweza kwenda kupunguza na kuondoa migogoro hii ambayo inatukabili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine kubwa ambayo wananchi wengi wanajiuliza na mimi nikiwepo najiuliza. Hivi ni kwa nini inapotokea mwananchi kwa namna moja ama nyingine ama amekutwa kwenye shoroba au ameingia hifadhini au wanyama wamekufa, kwa nini inatumika nguvu kubwa na askari wa Jeshi la Uhifadhi, hivi ni kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ameongea vizuri sana Mheshimiwa Musukuma asubuhi hapa ni kwa nini ni mafunzo yao ndio yanawafanya kwamba ukimuona mtu ni sawa sawa umemuona jangili unamfyatua tu risasi au ni nini yaani kwanini nguvu kubwa sana inatumika? Haya mambo yanasikitisha sana, yaani iko namna ya kuangalia ama kulifumua jeshi hili kwa ujumla na kuangalia namna iliyobora ama sijui wapewe maelekezo ama wapewe mafunzo kwa upya ama kuangalia mafunzo yao. Nadhani hatua ya kwanza sio kutumia nguvu kubwa, tuone namna ambayo inaweza kama kweli mwananchi ana makosa kuna namna, ndipo ambavyo hata askari akimkuta mwizi hawezi kumpiga risasi hivi hivi si atamkamata atampeleka kituoni na hatua zingine zitaweza kuendelea. Kwa hiyo, nadhani hata jeshi hili liwe na namna bora ya kuhakikisha inakabiliana na migogoro hii kwa namna iliyo sahihi bila kumuumiza mwananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo langu la Karatu tunapakana na Hifadhi ya Ngorongoro, tuna changamoto kubwa sana ya wanyama kuingia kwenye vijiji vya wananchi. Tuna kata karibia sita ambazo tumekuwa na changamoto ya muda mrefu ya wanyama kutoka hifadhini na kuingia kwenye maeneo ya wananchi. Kama ambavyo nimeeleza kuna mtu mmoja leo amefariki na wengine kadhaa huko nyuma wamejeruhiwa na mazao kuweza kuharibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nafahamu kuna mpango kupitia bajeti ya mwaka huu ambayo inafanywa na Hifadhi ya Ngorongoro kujenga fensi ya umeme ya kilometa 30 ili wanyama wasianze kutoka kwenda kwenye maeneo ya hifadhi. Hili ni jambo jema sana tunawapongeza kwa hilo lakini kama haitoshi pia kuna vituo vya polisi vitajengwa takribani 15 kupitia fedha za mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kama ambavyo mmeweka kwenye bajeti yenu hiyo electrical fence ambayo mnataka kuweka tunaomba muweke kwenye vipaumbele yale maeneo ambayo ni korofi zaidi. Muyatangulize haya na maeneo mengine yaweze kufuata lakini pia Mheshimiwa Waziri unaweza kuchukua sample hii ya Ngorongoro kupeleka kwenye maeneo mengine Nchi nzima ambapo kwa kiwango kikubwa wanakabiliana na changamoto hii ya wanyama kutoka kwenye maeneo ya hifadhi kwenda kwenye maeneo yao kwa kuweka hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najua ni gharama kidogo lakini ifike mahali hichi tunachokipata kutokana na Sekta hii ya Utalii irudi kwa wananchi kwa kuwapa unafuu, kwa kuweka hizo fensi ili wananchi waendelee kuishi kwa amani katika maeneo yao. Mifano mizuri mnaweza kwenda kujifunza hata South Africa wanatumia sana hii ili kuhakikisha wanyama wanabaki salama kwenye eneo la hifadhi lakini mwananchi kwenye eneo lake nalo anabaki salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwapongeze sana Ngorongoro kwa hatua hii tunamba basi mtekeleze ili Wananchi wa Karatu kwenye haya maeneo waweze kuishi salama katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala liliotokea juzi Mto wa Mbu, eneo la Jangwani. Mheshimiwa Waziri nimekusikiliza pia kwenye hotuba yako, nimesikitika kidogo. Kwanza mpaka leo vijana wawili ambao walikutwa kwenye ziwa na askari wa uhifadhi ambao walifungwa pingu walipigwa, mpaka leo hawajulikani walipo. Tunaomba mtuambie hawa vijana wako wapi familia zao zinalia, zinawatafuta kijana mmoja ni wa Karatu na kijana mwingine ni wa Mto wa Mbu. Vijana hawa mpaka leo hawajulikani, tunatamani kujua na wanatamani kujua na Mheshimiwa Waziri ikikupendeza uende ukae na hawa wananchi wa maeneo haya uwaambie na uwasikilize, kwa sababu kwenye hotuba yako umesema hawa wananchi walikuwa wanavamia walikuwa wanavamia boti ya askari wa uhifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sikiliza, askari wa uhifadhi wana boti za umeme, wananchi wa kawaida wanabodi za kawaida. Hivi inakuaje yaani mwenye boti ya kawaida ambaye haina nguvu na huyu mwenye boti ya umeme eti huyu wa umeme anatishiwa na mwingine, how come? Yaani haingii akilini. Mkatuambia hapa juzi kuna wananchi wameondoka na pingu, hivi askari wale wa Jeshi la Uhifadhi wana bunduki na mitutu, kuna mwananchi atathubutu kwenda kumchukulia hiyo pingu wakati amebeba hizo silaha, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba haki za wananchi hawa familia hizi zinalia halafu msiseme uongo pale ambapo pana ukweli mseme muombe radhi kwa sababu makosa yanatokea hakuna aliyemkamilifu, muombe radhi mseme ukweli, mzifikie familia hizi, msikie kilio hichi kilichofanyika ni unyama wa kupitiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na hawa vijana wawili waliopotea, wawili wamefariki wengine bado majeruhi, kwa nini haya? Ndio haya nasema kwa nini inafikia askari hawa wa Jeshi la Uhifadhi wanatumia nguvu kubwa kukabiliana na wananchi pale ambapo inatokea hii changamoto? Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri ikikupendeza na kama utaona inafaa basi watembelee wananchi hao ukutane nao, usikie kutoka kwenye midomo yao itakuwa vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala mengine mawili kwa haraka haraka nimesikia kengele imegongwa. Suala moja ni mamlaka ya usimamizi ya wanyamapori TAWA. Hii TAWA imeanzishwa kwa amri ya kisheria chini ya kifungu cha nane cha Sheria ya Uhifadhi ya Wanyamapori na ina bodi ya ushauri haina bodi ya kiutendaji. Huko nyuma Kamati imeshauri mara nyingi sana iletwe sheria hapa Bungeni ya kuhakikisha TAWA inaundwa properly kwa mujibu wa sheria. Tuonaomba Mheshimiwa Waziri utapitia ripoti za Kamati utaziona, tunaomba TAWA ipewe mamlaka yenye nguvu kwa sababu ina kazi kubwa ya kusimamia mapori mengi ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine Ziwa Manyara, Ziwa Manyara linaendakwisha na linaenda kupotea kabisa kwa sababu ziwa lile limejaa tope, maji hata yakiingia pale yakae muda mrefu. Mwisho wa siku tutaipoteza Hifadhi ya Manyara, tunaomba sana zifanyike jitihada za kuhakikisha Ziwa Manyara linakombelewa na linarudi kwenye hali yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, …tunaomba ujenzi wa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ujenzi wa Barabara ya Serengeti, barabara ile haipendezi kwa wageni wanaofika kwenye eneo hili. Tunaomba mlifikirie mjenge kwa namna iliyobora bila kuharibu mazingira bila kuleta athari yeyote kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Naomba nitoe mchango wangu mfupi hasa kuhusiana na suala zima la hali ya uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukipitia taarifa ya tathmini ya MDG kwa nchi yetu kuanzia mwaka 2000 hadi 2015, taarifa inaonyesha kwamba uchumi wetu umekua kwa asilimia saba kwa kipindi cha miaka 15. Lakini taarifa hiyo inaonesha kwamba kama uchumi utakuwa mfululizo kwa asilimia saba kwa miaka 15 maana yake inategemewa suala la umaskini utapungua kwa kiwango cha asilimia 50. Lakini taarifa hiyo inaonyesha kwa Tanzania imepungua kwa asilimia kumi tu, kwamba bado tuna safari ndefu ya kufikia hicho kinachoitwa uchumi wa kati ambayo ni dira ya Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukisema suala la ukuaji wa uchumi lazima pia tuangalie sekta zingine ambazo zinaweza kuchochea suala zima la ukuaji wa uchumi, bado tuna safari ndefu. Ukiangalia kwenye sekta tu ya kilimo uchumi unakua kwa asilimia mbili tu na tunajua kabisa suala la kilimo ni tegemeo kwa Watanzania wengi, wanategemea ili kuondokana na umaskini.
Lakini sekta hiyo imekua kwa asilimia mbili tu kama ambavyo taarifa hiyo inaonyesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la ukuaji wa uchumi Serikali mkija hapa na figures na kujigamba mkisema kwa ujumla wake inakuwa kwa asilimia saba bila shaka mtakuwa mna wahadaa wananchi lakini kwa uhalisia ukienda kwenye sekta moja moja ambazo zinachochea uchumi huo bado tupo nyuma na tuna hali ngumu. kwa hiyo, ni vizuri sana mnaposema suala hili la uchumi muangalie uhalisia wa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisema pia suala la uchumi tukiangalia hali ilivyo sasa kuna mdororo mkubwa wa uchumi, hakuna mzunguko wa fedha, hakuna fedha katika hata bajeti tuliyopitisha ukiangalia sasa tunaingia kwenye quarter ya pili hata asilimia 26 ya utekelezaji wa bajeti bado hamjafikia na kama mmefikia ni hiyo asilimia 26 tu. Kwenye Serikali za Mitaa hakuna fedha, kwenye taasisi za umma hakuna fedha, Wizarani tumeona taarifa mbalimbali Wizara zikiwasilisha kwenye Kamati hakuna fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ni mbaya, hakuna fedha, nini kipaumbele? Mna mpango gani wa kufikia hiyo bajeti ambayo tumeipitisha kwa shilingi trilioni 29 katika mwaka huu. Lakini mnafanya projection ya bajeti ya shilingi trilioni 33 kwenye bajeti ijayo. Napata mashaka sana kama hii tu ya sasa utekelezaji wake tunaingia kwenye quarter ya pili bado hali ni mbaya halafu unafanya projection ya shilingi trilioni 33 kwenye bajeti ijayo tafsiri yake ni kwamba mnajifurahisha ninyi kama Serikali kwa namba hizi kubwa kubwa, lakini mnawaongezea wananchi mzigo wa kuendelea kulipa kodi.
Kwa hiyo, unaona kabisa ni bajeti ambayo kwa kweli mwisho wa siku haitaweza kutekelezeka ipasavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mmeeleza katika mpango huu kumekuwa na changamoto mbalimbali za kuweza kufikia mipango hiyo. Mojawapo mmesema ushiriki mdogo wa sekta binafsi lakini pia kuna suala la upatikanaji wa mitaji ya uwekezaji. Hivi hizi sekta binafsi kama hazijatengenezewa mazingira rafiki, kama hizi sekta binafsi hazijawa na imani na Serikali iliyopo madarakani kwa sababu tumeona wakati mwingine mna ndimi mbili mbili sekta binafsi ataogopa ku-invest hela zake kwasababu hajui Serikali kesho inatamka nini? Inafanya nini? Kesho inakuja na kodi gani? Kama msipoweka haya mazingira mazuri hakuna sekta binafsi atakayeweza kuja kuwekeza katika nchi hii kama ambavyo nyie wenyewe mmekiri hapa ni changamoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, bado tunahitaji kuwepo na sera na mazingira rafiki ya kuweza kuhakikisha hizi sekta binafsi kwa kweli zinakuwa na wao ni sehemu ya uchumi wa nchi hii. Mmeeleza pia changamoto nyingine ni upatikanaji wa mitaji ya uwekezaji, hili pia ni changamoto kweli kwa sababu kama sasa hivi mabenki hali ni mbaya, mabenki mengine yameshakua chini ya usimamizi wa BOT, mabenki hayana mzunguko wa fedha, fedha ambazo zilikuwa za Serikali kwenye commercial banks zote zimehamishiwa BOT, obviously hakuna uwekezaji unaweza kufanyika. Kwa hiyo, bado tuna changamoto kubwa sana ambayo kwa kweli itakuwa ni ngumu sana kuweza kufikia hicho kinachoitwa uchumi wa kati ambayo ni dira ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona hali ilivyo sasa hivi, lakini wakati mwingine unajiuliza hivi kuna haja gani ya kujadili pia mpango au kujiwekea mpango wakati mpango wenyewe ukienda kwenye utekelezaji hauwezi kufanyiwa tathmini na kuona matokeo. Lakini kuna vitu vingine ambavyo vinaenda kutekelezwa ambayo hayapo kwenye mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu ambao tunaumalizia 2016/2017 suala la kuhamia Dodoma halikuwepo lakini Rais amelitamka limetekelezeka, halikuwepo kwenye mpango na kuhama Dodoma sio kazi ndogo, inahitaji fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini angalau sasa hivi mmeiweka kwenye mpango unaokuja; sasa unaona wakati mwingine kama tunaendeshwa kwa matamko ya namna hii ambayo hayapo kwenye mipango maana yake unaenda kuharibu bajeti ambayo imepitishwa hapo. Kwa hiyo, pia wakati mwingine ni lazima haya ambayo mnayatamka ni lazima yaendane na bajeti ambayo tumeipitisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimuulize Waziri wa Fedha na anisaidie majibu atakapohitimisha. TRA wamesema wanakusanya 1.3 trillion kila mwezi, hiyo ni projection. Mishahara inayolipwa nchi hii ni shilingi bilioni 540, madeni ya ndani ama ya nje inalipwa shilingi bilioni 900, ukifanya hapo mahesabu ni kama one point four trillion na makusanyo ni 1.3 trillion kila mwezi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuuliza hizo ndege zilizonunuliwa kwa fedha cash hii hela mliipata wapi? Wakati mnachokikusanya TRA kila mwezi ni 1.3 trillion, ukilipa madeni, ukilipa mishahara ni 1.4 trillion; fedha za kununua ndege kwa hela cash mmeipata wapi? Naomba Mheshimiwa Waziri unijibu ama ni hizo fedha zilizopo BOT ambazo zimekusanywa na taasisi zikawekwa kule mkaenda mkazichukua mkanunua ndege cash? Naomba nipate majibu ya suala hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala lingine ni kuhusu suala zima la elimu. Wakati nimechangia kwenye bajeti ya elimu hapa mnajivunia leo suala la elimu bure, lakini elimu bure hii ni bure tu kwa sababu hawalipi kile ambacho kinatakiwa. Ukienda kwenye uhalisia wa shule zetu hali ni mbaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi mmesema mwanzoni wakati wa awamu ya JK mliagiza kujengwe maabara nchi nzima; wananchi wakajichanga, mkaita wadau mbalimbali wakachanga maabara ikajengwa, yamebaki majengo yameachwa. Mmeyaacha yale majengo hayana vifaa, maabara hayafanyi kazi ni majengo tu yaliyosimama mkahamia kwenye madawati mmetangaza madawati nchi nzima watu wametengeneza madawati mengine hayana standard, hayana quality inayotakiwa leo mnataka kukimbilia kujenga madarasa kwa mfumo ule ule wa kulipuka. Kule mmeshasahau maabara, madawati mengine hayana kiwango, leo mnakurupuka mnaenda kujenga…
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema muache kukurupuka, mkianzisha jambo moja likamilike, liwe na manufaa, lianze kufanya kazi muende kwenye jambo lingine, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na namshukuru Mheshimiwa Mwakajoka kwa kunipa dakika tano. Nami nianze kuchangia kwenye suala zima la mamlaka makubwa ambayo nafikiri RC na DC na DAS wanazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafurahi sana kuona leo kwa sababu mwaka jana hapa wakati sisi Wabunge wa Kambi ya Upinzani tunajaribu kuonesha matatizo na changamoto na udhaifu ambao baadhi ya RC na DC wanayo katika maeneo yetu, tulibezwa hapa, hatukusikilizwa lakini leo humu baadhi ya Wabunge wa CCM nao wameona hiyo shida na wameanza kusema. Nafikiri huu utakuwa ni mwanzo mzuri ili tuendelee kuelewana sawasawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema kwamba hawa RC na DC wamekuwa Miungu watu, wameona kwamba wana mamlaka makubwa kuliko mtu yeyote, hawatambui nafasi za Wabunge, wanaweza ku-revoke maamuzi ya Baraza na kuyaingilia, hata pale ambapo hayastahili. Ifike mahali hizo semina elekezi ambazo mlizisema zimefutwa nadhani iko haja ya kurudisha na kukaa na hao watu na kuwaambia. Siyo semina tu, hata akili nyingine tu ya kawaida ya busara ya RC au DC kujua mipaka yake, kujua namna ya kushirikisha hawa watu hawana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima muangalie mfumo mwingine, sijui wateuliwe wengine au wafanye nini hawa wameshindwa kazi, wamekuwa Miungu watu. RC anakaa kwenye kikao anaongea anasema, nadhani mnaelewa hapa kuna Waziri naweza kuwa na maamuzi makubwa kuliko Waziri hata Waziri mwenyewe anaelewa, anasema kwenye kikao na Waziri yupo, huyu ni RC. Sasa kama wanasema vitu kama hivi mbele ya Mawaziri unategemea nini kwa Wabunge?(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, RC anakuja kwenye eneo lako, Wabunge mnaomba kuonana nae hana muda na Wabunge. Haya ni masikitiko, lakini sasa angalau tunaanza kuelewana humu ndani na angalau haya machungu na ninyi Wabunge wa CCM mmeanza kuyapata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utawala wa sheria; sioni sasa kama kuna utawala wa sheria. Kuna Mbunge mmoja ameongelea kuhusu mlundikano wa kesi au mlundikano wa wafungwa Magerezani, lakini leo kama kuna kesi ya uchochezi ya mwana CHADEMA haichukui miezi mitatu hukumu tayari na inasikilizwa haraka sana, lakini kuna watu wamekaa gerezani kwa kesi ama za kusingiziwa au ambazo siyo za kisingiziwa miaka tisa, miaka 10, miaka mitano, miaka miwili wanasema upelelezi bado, lakini mwana-CHADEMA akisema jambo tena anaambiwa mchochezi na hii tafsiri ya uchochezi itabidi mtuambie uchochezi ni nini maana yake neno uchochezi linatumika vibaya, anaambiwa ni mchochezi, anapelekwa Mahakamani haraka hukumu miezi sita, miezi nane, miezi mitatu jela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sidhani kama kuna utawala wa sheria, ni lazima mjitafakari upya, muangalie kama tuna Katiba, kama tuna sheria, kama kweli kuna kutenda haki kwa nini haki inatendeka kwa watu wachache na watu wengine wananyanyaswa kwa sababu ni washabiki wa upande fulani au wa Chama fulani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie suala la mwisho kuhusu Madiwani; Madiwani wamekuwa ni Wasaidizi wetu hata sisi Wabunge kwa maana kama tukiwa hapa Bungeni kwenye vipindi virefu vya Vikao vya Bunge, wao ndiyo wamekuwa wakikaa na wananchi na wakiwasikiliza kero zao, lakini Madiwani wamesahaulika. Madiwani leo wanapewa posho ya sh. 350,000 basi na hizo posho za vikao, tena wako Wakuu wa Wilaya wengine wanafuta posho za Madiwani ambazo zingine ziko kwa mujibu wa taratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Wakuu wa Wilaya wengine wanasema posho hii haitakiwi, hii haitakiwi, kweli kuna zile ambazo haziko kwa mujibu wa taratibu, lakini zile zilizoko kwa mujibu wa taratibu DC wanaingilia, wanazifuta. Tumewasahau Madiwani, hatufikirii kuwaongezea posho zao, tumewaacha Madiwani hawapewi mafunzo, capacity building haipo tena, angalau kwenye awamu zilizopita walikuwa wanapewa. Sasa unampeleka Diwani asimamie mradi wa mabilioni, yuko kwenye Kamati ya Fedha lakini hajajengewa uwezo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2017/2018 unaonyesha kwa kiwango kikubwa Serikali inategemea kukopa fedha katika mifuko hii ili kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, kukopa sio dhambi, lakini mikopo ambayo inazidi uwezo na kupelekea hatari ya kuua/kufifisha uwezo na kupeleka hatari na lazima Serikali ituambie imejipanga vipi kuhakikisha mifuko hii haifi/kupunguza uwezo wake?
(a) Je, return on investment kwa miradi ya namna hii ambayo inachukua muda mrefu kurudisha faida imetazamwa kwa kiwango gani?
(b) Je, foreseeable risk kwenye operation za viwanda na miradi inayowekezwa imefanyika assessment kina?
(c) SSRA ambaye ni mdhibiti na msimamizi wa mifuko hii inaweka ukomo/kiwango kwa mifuko kutokopa zaidi ya 20%. Hata hivyo kwa taarifa ya Benki Kuu ya mwaka 2016 inaonyesha kuwa proportion ya mifuko kwenye deni la ndani ni 26% kutoka 16% na imechukua nafasi ya mabenki ya biashara. Uhai wa mifuko hii upoje? Kwa nini Serikali iendelee kukopa zaidi kinyume na sheria zilizopo?
(d) Kumekuwa na hoja ya muda mrefu wa kuunganisha mifuko hii ya hifadhi ya jamii. Je, lini Serikali itaanza machako wa kuunganisha mifuko?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, usikilizaji wa mashauri mahakamani; pamoja na Serikali kueleza 80% ya mashauri yameweza kusikilizwa, kasi hii bado inahitaji kuwekewa nguvu zaidi ili kuendelea kupunguza mrundikano wa kesi zilizopo mahakamani. Serikali lazima itie nguvu na mkazo katika Mahakama za Mwanzo na Mahakama za Wilaya kwani huko ndiko kwenye mrundikano wa kesi nyingi, jambo ambalo linawafanya wananchi wenye kesi mbalimbali kuendelea kutumia muda mwingi mahakamani. Hata hivyo, haki inayocheleweshwa ni sawa na haki iliyonyimwa. Nashauri Serikali iendelee kujipanga kuhakikisha mrundikano wa kesi katika mahakama za chini zinakwisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo; pamoja na umuhimu wa Taasisi hii ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo, ipo haja ya kuongeza chuo hiki katika kanda nyingine za nchi hii. Ni ukweli kuwa nchi hii ni kubwa na wanafunzi wanaohitaji kupata mafunzo haya ni wengi. Hivyo basi, ni muhimu kwa Serikali kuongeza vituo vya mafunzo hayo kwa angalau Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Kati, Kusini na Magharibi. Kwa kuongeza vituo hivyo itasaidia wanafunzi kumudu gharama za mafunzo na hivyo kuongeza wanafunzi zaidi.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upungufu wa dawa nchini; kumekuwa na upungufu wa muda mrefu wa dawa hapa nchini, tatizo hili limekuwa la kudumu na kwa kuwa chanzo kikubwa cha fedha kwa ajili ya kununua dawa inategemewa na mapato ya makusanyo ya kodi mbalimbali hapa nchini. Hata hivyo, kumekuwa na mifuko ambayo inaanzishwa na chanzo cha mapato kwa ajili ya mfuko huo unakuwa wa uhakika na kuleta ufanisi unaokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano ni Mfuko wa Barabara, Miradi ya REA ambayo chanzo cha mapato inatokana na fedha za mafuta na mfuko huo fedha zake haziguswi (ring fenced). Kwa kuwa dawa ni suala muhimu sana kwa ajili ya maisha ya Watanzania, hivyo ni wakati muafaka sasa Serikali ianzishe mfuko maalum wa dawa na fedha zake zitokane na chanzo cha uhakika ili kupunguza na kuondoa kabisa tatizo la ukosefu wa dawa hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Taifa ya Mount Meru; Hospitali hii ndiyo hospitali inayotegemewa katika Mkoa wa Arusha, hata hivyo kuna changamoto katika utoaji wa huduma kwa vifaa muhimu kama x-ray machine kuharibika mara kwa mara. Serikali ione umuhimu wa kuiwezesha kwa kiasi kikubwa hospitali hii ambayo ni muhimu kwa Mkoa wa Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni motisha kwa watumshi wa afya. Watumishi wa afya nchini ni kada muhimu sana ambayo wameamua kufanya kazi kubwa ya kutoa huduma kwa Watanzania wote. Hata hivyo, suala la afya ni muhimu sana kwa ustawi wa nchi yetu. Serikali lazima itazame kwa upya maslahi ya watumishi wa afya hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wazee; kumekuwa na ahadi ya muda mrefu ya Serikali kuwa itaboresha makazi ya wazee, jambo hili limekuwa linaandikwa kwenye vitabu bila utekelezaji. Wazee ni hazina ya nchi, tunapaswa kuwaenzi na kuwahudumia. Serikali ijipange vizuri ili kuhakikisha makazi ya wazee yanaboreshwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia kuhusu fidia kwa wananchi. Katika maeneo mbalimbali ya nchi ambapo Hifadhi za Taifa zimepakana na vijiji ambavyo wananchi wanaendesha shughuli za kilimo kumekuwa na changamoto za wanayama kuharibu mazao ya wananchi na wananchi hawapewi fidia kutokana na uharibifu huo. Kilio hiki cha wananchi kimekuwa cha muda mrefu na wakati mwingine hata kama fidia inatolewa kwa kuchelewa sana na kuleta usumbufu mkubwa kwa wananchi. Hivyo basi naishauri Serikali ifanye yafuatayo:-

(a) Kulipa fidia kwa wakati; na

(b) Malipo ya fidia yalipwe na mamlaka husika ambapo uharibifu umetokea kwani kwa kufanya malipo ya fidia kuwa central kwa maana ya kulipwa na Wizara imekuwa na usumbufu mkubwa na kuchelewesha malipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu migogoro ya vijiji na hifadhi za wanyamapori; migogoro ya wananchi na mipaka au hifadhi za wanyamapori imekuwa ya muda mrefu bila kupatiwa ufumbuzi, matokeo yake Serikali imekuwa ikikimbilia kuunda tume ya kufuatilia migogoro bila mafanikio. Nashauri ije na mkakati wa namna gani inamaliza migogoro hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sekta ya misitu, natambua umuhimu wa misitu na tunaunga mkono juhudi na jitihada za kulinda misitu. Miongoni mwa mazao ya misitu ni mkaa ambayo ni nishati muhimu sana kwa wananchi kwa ajili ya matumizi ya kupikia. Wizara imetoa katazo kuwa mkaa usitoke nje ya Wilaya. Katazo hili limekuja bila kuwepo na nishati mbadala kwa wananchi hao. Miji ambayo haina sasa watakosa nishati ya mkaa na wananchi hawawezi kumudu gharama za gesi. Nashauri Serikali ifute katazo hili huku tukiwandaa wananchi kutumia nishati mbadala ambayo wataiweza na kuimudu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Nianze mchango wangu kwa sekta nzima ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya utalii imekuwa ikichangia asilimia 17 ya Pato la Taifa ukilinganisha na sekta zingine. Kwa tafsiri nyingine unaweza ukasema Pato la Taifa chanzo chake kikuu ni sekta ya utalii. Sekta hii ya utalii imekuwa na changamoto nyingi ambazo zinazidi kuongezeka. Kama changamoto ni nyingi na zinazidi kuongezeka maana yake sekta hii haiwezi kukua na kuendelea kuongeza Pato la Taifa kwa maana ya kutoka kwenye hiyo asimilia 17 kwenda hata angalau asilimia 20.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa changamoto zilizopo kwenye sekta hii, imekuwa haitiliwi mkazo kutangazwa ipasavyo. Mikakati ipo lakini inawezekana fedha zinakosekana ya kutangaza kwa upana sekta ya utalii ndani na nje ya nchi, imekuwa ni changamoto ya muda mrefu ndio maana tunabaki palepale hatuwezi kwenda mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine Serikali haina ubunifu wa kuongeza vivutio vingine vipya. Tumekuwa na vivutio vya zamani na hivyo vingine vimetelekezwa, lakini hakuna ubunifu wa kuwa na vivutio vipya ambavyo vitawashawishi watalii waweze kuja kuangalia kwa wingi hapa nchini. Kwa hiyo, ni wajibu wa Serikali kuangalia namna gani vivutio vilivyopo mnaviendeleza, lakini mnabuni vivutio vingine ambavyo vitaweza kuhahakisha kwamba watalii wanakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo linaifanya sekta hii ya utalii iwe na changamoto kubwa ni masharti magumu kwa wawekezaji ikiwemo suala la kodi. Katika Awamu ya Nne kodi ambazo zilikuwa zinalipwa na wawekezaji katika sekta ya utalii ilikuwa ni kodi kati ya 14 mpaka 16. Leo Serikali ya Awamu ya Tano mmeingia madarakani mmepandisha kodi ambazo wanalipa wawekezaji katika sekta ya utalii zimetoka 14 mpaka 36 na sasa hivi ninasikia tena mnataka kupandisha nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hizi au namna gani kama mnaongeza kodi hakuna mwekezaji ambaye atakuja ku-invest kwenye sekta ya utalii na tukaona inakuwa atakuwa anazikimbia hizi kodi. Kwa hiyo, tunatarajia kwamba muende mkae, mpunguze kodi muweze ku- encourage wawekezaji wengi ili sekta ya utalii iweze kukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine katika haya haya masharti magumu, leo mtu akitaka kupata TALA licence unalipa dola 2000 kwa magari kuanzia matatu. Tunajua huko huko nyuma ilikuwa ni magari matano unalipa dola 2000, mkapunguza mkafanya magari matatu kwa dola 2000, lakini kwa wale vijana wa Arusha ambao maeneo yenye utalii atapambana atapata magari matatu atalipa dola 2000, huyu anashindana na mwekezaji mkubwa mwenye magari 100 naye analipa dola 2000. Kwa mfano, Leopard Tours wana magari kibao, naye analipa TALA licence ya dola 2000. Halafu kijana wa Arusha anajitahidi amepata magari matatu naye analipa dola 2000. Kwa nini Wizara msifikirie kupunguza hii TALA licence mkalipa TALA licence kwa gari ambayo itaiingizia Serikali mapato zaidi; yule mwenye magari 100 atalipa kulingana na idadi yake ya magari na yule mwenye magari matatu naye atalipa kulingana na idadi yake.

Mheshimiwa Waziri hii limekuwa ni kelele ya muda mrefu lakini hatupati majibu ya kuwasaidia hawa. Pia itawasaidia na ninyi kuongeza mapato, kwa hiyo, ni vizuri mkalifikiria hilo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine katika sekta ya utalii ni ushiriki mdogo wa maonesho ya utalii na kutokupewa kipaumbele. Masuala mazima ya maonyesho ya utalii na vivutio vya utalii inaoneka imeachiwa sekta binafsi na Serikali imekaa pembeni, imekuwa ni changamoto ya muda mrefu. Sasa kama ninyi mkaa pembeni mnaziachia sekta binafsi ziende zenyewe zijitangaze, zijipambanue na kuonesha wana vitu gani, ni kwa namna gani sekta hii itaweza kukua. Haiwezi kukua obviously kutakuwa kunaendelea kuwa na changamoto hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ni vyuo vichache vya utalii vinavyotoa mafunzo ya utalii na imekuwa ikitoa mafunzo duni haiendani na kasi ya ukuaji wa utalii. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali mkafikiria namna gani kushirikiana na sekta binafsi kuhakikisha kwamba vyuo vya utalii vinakuwa na ubunifu zaidi, lakini inaendana na kasi ya ukuaji wa utalii duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la migogoro ya vijiji na hifadhi za wanyamapori. Migogoro hii imekuwa ni migogoro ya muda mrefu, ni migogoro ambayo ndani ya Bunge tumekuwa tukisema lakini unachokiona tukipiga kelele kuhusu migogoro, Serikali mnakimbilia kuunda Tume. Mnakimbilia kuunda Tume, mnatuahidi kwamba Tume zikifika maeneo hayo mtashirikisha wadau mbalimbali, wanafanya kazi hizo wanamaliza hatujawahi kusikia ripoti ya Tume hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2009 Bodi ya TANAPA iliunda Tume ya kuchunguza migogoro ikatoa mapendekezo, sijui yamefanyiwa kazi kwa kiasi gani. Mheshimiwa Waziri Mkuu wa zamani Mheshimiwa Mizengo Kayanza Pinda aliunda Tume, Mheshimiwa Kagasheki akiwa Waziri aliunda Tume, Mheshimiwa Lukuvi aliunda Tume na sasa hivi nasikia mmeunda tena Tume inayohusisha sekta zote lakini hakuna majibu. Serikali mkisikia migogoro ya wananchi na hifadhi badala ya kutuletea majibu mnakimbilia kuunda Tume zinazotumia fedha nyingi za walipakodi, taarifa ya Tume mnaweka kapuni hamtuambii. Leo hapa msimame mtuambie angalau ni mgogoro gani ambao mmeumaliza? Hamna na migogoro inaendelea! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kila siku kuona wananchi wanashughulikia tu migogoro wanaacha shughuli zingine, Serikali mnakimbilia kuunda tume ambazo hatupati majibu yake. Kwa hiyo, nafikiri ni wakati muafaka sasa Serikali mtuambie kwanza hizi Tume zote ambazo mmeziunda majibu yake yako wapi? Ripoti yake iko wapi? Utekelezaji wa matokeo ya Tume hizo umefanyika kwa kiwango gani? Kwa nini kama ambazo hazijafanyika ni kwa nini imeshindikana kufanyika mpaka sasa hivi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la mgogoro wa Loliondo. Mgogoro wa Loliondo pia ni kati ya migogoro ambayo imekuwa ni ya muda mrefu. Leo Serikali inataka kuondoa wananchi takribani 54,000 katika vijiji 14 waondoke kwenye eneo la kilometa za mraba 1,500, hivi unawaondoa watu 54,000 unawapeleka wapi? Huko unakowapeleka si ndiyo unaenda kuendeleza mgogoro mwingine wa ardhi? Serikali mtuambie mna maslahi gani na suala la Loliondo, kwa nini mmeshindwa kulipatia ufumbuzi wa muda mrefu? Kwa sababu umekuwa ni mgogoro wa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, badala mtuletee ufumbuzi wa tatizo la Loliondo, mnakimbilia mnasema NGO’s zilizoko Ngorongoro zinachochea wananchi kuendeleza migogoro hii. Kwanza hizi NGO’s zilizo nyingi zimesaidia kujenga uelewa wa wananchi wa kule, lakini kama kweli kuna NGO’s ambazo zinafanya ushawishi na uchochezi it is okay zichukuliwe hatua lakini siyo kuzihukumu NGO’s zote labda kwa sababu ya baadhi ya NGO’s ambazo zinafanya ndivyo sivyo.

Kwa hiyo, Serikali mtuambie hivi mna maslahi gani na huyu Mwekezaji wa Loliondo huyo OBC huyu Mwarabu mtuambie? Huu mgogoro umekuwa wa muda mrefu, mnaenda mnaunda Tume, sijui Waziri Mkuu ameunda Tume, sijui Waziri umeenda, Mkuu wa Mkoa Gambo ameenda, sijui ataenda na nani labda aje na malaika naye aende, lakini hamtupatii ufumbuzi, kwa nini wananchi wa Loliondo wanateseka kwa muda mrefu? Mtuambie Mheshimiwa Waziri kwanza mna maslahi gani na huyu Mwarabu na kwa nini mgogoro huu haumaliziki?(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwa dakika tano hizo katika Wizara hiyo ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niungane na Watanzania wote kutoa pole nyingi sana kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha kufuatia ajali ambayo imechukua maisha ya watoto wetu, walimu pamoja na dereva iliyotokea Wilaya ya Karatu Wilaya ambayo ninatokea, Mkoa wa Arusha ambao ninauwakilisha. Poleni sana na Mwenyezi Mungu azidi kuwapa nguvu familia. Pia nitoe pole kwa wazee wetu hawa ambao wametangulia mbele ya haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mchango mfupi kuhusiana na Wizara hii kwa sababu pia ya muda. Taifa lolote ambalo linachezea elimu ni Taifa ambalo linaenda kuangamia na Taifa ambalo linaenda kupotea. Nasema hivi kwa sababu kumekuwa na utamaduni kila Waziri anayekuja kwenye Wizara hii anakuja na style yake ambayo ama anafikiri inaenda kuboresha elimu au inaenda kuangamiza elimu kabisa.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Mama Ndalichako umeingia hapa wewe, wewe ni mtaalam, hujawahi kuwa mwanasiasa, tunaamini utaenda kuweka mifumo thabiti, mifumo itakayoboresha elimu kwa watoto wetu, mifumo ambayo itawaandaa watoto wetu kuwa na Taifa ambalo litaendelea kuwa Taifa kama ambavyo nchi nyingine tumeona. Tunategemea utaenda kuweka mifumo ambayo hata wewe ukiondoka kesho, Waziri yeyote atakayekuja hataenda tena kucheza na elimu ya watoto na hataweza kwenda kucheza na elimu ya Watanzania. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ndalichako tunategemea utaenda kuweka hiyo mifumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie kuhusu mfumo wa mpango wa elimu bure. Serikali imekuwa ikitamba sana kuhusu suala la elimu bure na imesema imefanikiwa. Ukweli sio sahihi. Huwezi kuangalia mafanikio ya elimu bure kwa kuangalia idadi ya watoto waliojiandikisha, ndiyo mmekuwa mkisema hivyo. Idadi ya watoto waliojiandikisha kuanza darasa la kwanza kweli inaongeza, lakini hiyo sababu pekee ya kutamba ya kujigamba na kusema eti elimu bure imekuwa na matokeo chanya kwa Watanzania siyo kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna changamoto nyingi, kuna changamoto nyingi sana katika suala zima la elimu katika nchi hii, ambapo pia taarifa ya Kamati imeonesha. Kwa hiyo, tunategemea ama mje na mfumo mwingine wa kusema kabisa, ama mmeshindwa hiyo elimu bure kutoa, ambayo mnaita elimu bure kwa sababu hizo changamoto au muondoe hilo neno au muwaambie sasa Watanzania kwamba tulisema elimu bure, lakini kuna changamoto, tunahitaji kuwa-engage Watanzania na wao katika suala zima la kuondoa changamoto za elimu hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu wanafunzi waliopata mimba na kurudishwa mashuleni. Hatuelewi ni kwa nini kuna kigugumizi kuhusiana na watoto wa kike waliopata mimba wananyimwa kurudi shuleni. Mheshimiwa Kakunda amechangia hapa asubuhi, yeye ni mtaalamu mzuri sana, amekaa kwenye system muda mrefu anapinga hili jambo. Hivi, watoto wanapata mimba, hawarudi shuleni, hivi tunazidi kuondoa ujinga au tunazidi kuzalisha ujinga? Kwa sababu hawa watoto wanapata mimba wapo wanaobakwa, wapo ambao kweli inawezekana mazingira yanawalazimisha, wako wengine ambao tu ni watundu wanakuwa kwenye hiyo hali wanapata mimba. Hivi kupata mimba na kuzaa ni dhambi? Wavulana walowapa mimba wanaendelea, hawa watoto wa kike waliopata mimba wanarudi majumbani. Tunaendelea kuzalisha ujinga kwa Watanzania, na hatujui ni kwa nini Serikali mnapata kigugumizi. Mbona wenzetu wa Zanzibar wanaendelea hawa watoto wakipata mimba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bunge la Kumi nilikuwa na Kamati ya Huduma za Jamii tulikuwa tunasimamia Wizara ya Elimu tulienda Zambia, wanarudi mashuleni watoto hawa. Kwa nini kwa Tanzania? Kwa nini mnapata kigugumizi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wewe ni mama, wewe ni mwanamke mwenzetu, tuwaonee huruma watoto wetu wa kike ambao wako kule vijijini wanapata mimba, wanarudishwa majumbani, hawawezi kuendelea na shule, halafu watoto wa kiume waliowapa mimba wao wanaendelea na shule.

Waheshimiwa Wabunge wanawake, Waheshimiwa Wabunge, Wajumbe wa TWPG, Wizara hii bajeti yao isipite mpaka tupate kauli ya Serikali ni lini wataruhusu watoto waliopata mimba waweze kurudi mashuleni. Kwa hiyo, tunategemea Mheshimiwa Waziri utakuja na majibu siku unahitimisha hoja yako na ujiandae kwa hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee Mabaraza ya Ardhi; mojawapo ya malengo ya kuanzisha mabaraza haya ni kupunguza migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali hapa nchini na pia kuharakisha usuluhishi wa kesi za ardhi. Pamoja na malengo haya mazuri mabaraza haya haiwezekani kutekeleza majukumu yake, ufanisi umekuwa mdogo kwa kukosa vitendea kazi, watumishi wachache wenye maslahi duni na kutopelekewa fedha za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa zaidi ipo katika Mabaraza ya Kata ambapo ndipo kuna kesi nyingi na hawapatiwi fedha za kuendesha shughuli zao. Serikali kuwaachia Halmashauri wawezeshe mabaraza haya ni kuzidi kuyadumaza mabaraza haya kwani Halmashauri zenyewe vyanzo vyake ni vya kusuasua na wakati mwingine hazina fedha kabisa kwani mahitaji ni mengi zaidi ya fedha hizo za own source katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali ifanye yafuatayo:-

Kwanza, kuyawezesha mabaraza ya Ardhi ya Wilaya ikiwa ni pamoja na kuongeza watumishi ili mabaraza haya yatimize majukumu yao kwa mujibu wa sheria; na

Pili, Wizara ichukue jukumu la kuyawezesha Mabaraza ya Kata kuliko kuziachia Halmashauri, kwani mapato ya Halmashauri hayatoshelezi. Sehemu ya fedha za kodi ya ardhi katika Wilaya husika kiasi fulani zibaki ili kuyawezesha Mabaraza ya Kata katika Wilaya husika.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika mpango huu uliowasilishwa na Serikali hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, napenda kushauri Serikali inapoleta mipango hasa kwenye miradi mikubwa, isiwe na miradi mikubwa mingi ambayo itagharimu fedha nyingi tena za mkopo, lakini matokeo yake inachukua muda mrefu. Ni vizuri mkawa na miradi michache, hata kama mtakopa lakini angalau iwe michache mwisho wa siku iweze kuwa na ufanisi. Kama ambavyo mmefanya hapa, kuna miradi mingi lakini ukiangalia hata mipango ya miaka miwili nyuma iliyopiata hivyo vivyo, mmekuwa na miradi mingi sana ambayo hata leo ukifanyia tathmini nafikiri hakuna hata mmoja ambao tayari umeshaanza kuonesha matokeo, lakini tena mmekopa maana yake mnaendelea kuendeleza Deni la Taifa.

Kwa hiyo, ushauri wangu ni bora muwe na miradi michache yenye matokeo ya haraka lakini itakayotumia fedha kidogo au hata kama ni nyingi lakini kwa ukopaji ambao utakuwa si wa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nichangie katika Sekta ya Utalii. Pato la Taifa asilimia 17.2 inachangiwa na Sekta ya Utalii. Maana yake ni kwamba asilimia 25 ya fedha za kigeni inatokana na utalii. Lakini ukiangalia hapo kwenye mpango ambao umewasilishwa na Serikali hamjatilia mkazo wa kutosha wa namna gani sekta hii ya utalii ambayo inaingiza kiwango kikubwa cha Pato la Taifa inawezeshwa ili kuhakikisha utalii huu ambao unaingizia fedha za kigeni nchi hii uweze kuendelea kwa kiwango kikubwa. Mfano, umesema hapa Mheshimiwa Waziri, kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato yanayotokana na utalii. Maana yake ni kwamba mmekuwa mkizoea kuendeleza kuongeza kodi kwenye sekta ya utalii au kwa watu ambao wanafanya biashara ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tuliwashauri hapa wakati tunapitisha bajeti kwamba mfute baadhi ya kodi zilizopo kwenye utalii, hamkufuta, wenzetu wa Kenya wakafuta, sisi hapa tukaongeza. Maana yake ni kwamba unaendelea kufanya sekta ya utalii ni ghali sana hapa nchini, mwisho wa siku mzungu au mtalii yeyote atachagua kwenda kwenye eneo ambalo ni rahisi na ataona vile vitu ambavyo anavitaka, kwa hiyo mkiwa mnashauriwa, Waziri mpokee ushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mtu anayewekeza kwenye hoteli za kitalii analipa kodi 46. Mheshimiwa Waziri ni vizuri sana muwe na kodi chache ili watu wengi waingie kwenye kuwekeza kwenye utalii ili tuendelee kupata wageni maana yake utalii utakuwa ni rahisi. Tulimshauri sana Mheshimiwa Profesa Maghembe kipindi hicho lakini hakusikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi nyingine ni ya TALA license, unalipa dola 2,000 kwa magari matatu. Uwe na magari 100 unalipa dola 2,000. Ni kwa nini msifanye kodi hii ikalipwa kwa gari? Ukilipa kwa gari maana yake utawa- encourage watu wengi wawe na magari, utalii utakua, ushindani utakuwa mkubwa, biashara itakua. Unalipa dola 2,000, magari 100; wale Leopard Tours Arusha, makampuni makubwa wana magari 100 mpaka 200 lakini analipa dola 2,000. Kijana wa Kitanzania aliyepambana amepata hela ana magari matatu analipa dola 2,000, hii ni nini Mheshimiwa Waziri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeishauri Serikali, tulimshauri sana Mheshimiwa Maghembe hapa hakusikia akaendelea kushukilia msimamo huo, nafikiri ni vizuri muangalie hilo. Lakini sekta hii ya utalii pia imeajiri vijana wengi ambao walikosa ajira lakini wameji-engage huku. Kwa hiyo, tunategemea kwamba jinsi ambavyo utalii utaongeza Pato la Taifa ndivyo ambavyo wawekezaji wataingia kwenye sekta hii, ndivyo ambavyo pia vijana wetu wengi watapata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu viwanda, Serikali ya Awamu ya Tano mliingia kwa nguvu kubwa sana mkasema nchi hii ni nchi ya viwanda, Tanzania ya viwanda. Lakini siku hizi wimbo huu umeanza kupotea, sijui mnaendeleaje, hausemwi kwa nguvu ile ambayo mlianza nayo mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na matamko ya kutafuta kiki za kisiasa. Mheshimiwa Waziri jana wamezindua, wanasema kila mkoa utajenga viwanda 100, maana yake mikoa 26 tunategemea kuwa na viwanda 2,600. Sasa hivi viwanda mnavyotamka, kwanza mtupe tafsiri yake, kwa sababu akija Waziri wa Viwanda anasema vyerehani vitatu kiwanda, akija mwingine anasema viwanda ni viwanda, mtupe tafsiri sahihi ya viwanda ni nini ili siku tunapowafanyia tathmini ya hivyo viwanda ambavyo mmekuwa mkiwaambia Watanzania tujue ni viwanda kweli au si viwanda. Kwa hiyo msitafute kutafuta cheap kiki za kisiasa kuwanufaisha Watanzania wakati sio sawasawa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, upelekaji wa fedha za maendeleo katika Hospitali za Mikoa imekuwa wa kusua jambo ambalo linakwamisha shughuliza za utoaji wa huduma katika maeneo mbalimbali hapa nchini kwa kuwa mahitaji ya fedha za maendeleo ni mkubwa katika sekta na maeneo mbalimbali, hivyo basi naishauri Serikali kuliko kugawa fedha za miradi ya maendeleo kwa mtawanyiko wa nchi nzima bila kuonesha matokeo ya haraka na miradi kubaki viporo. Nashauri fedha za miradi ya maendeleo kila mwaka ipelekwe kikanda kwa kuangalia na kutanguliza maeneo yenye mahitaji makubwa zaidi. Hata hivyo ugawaji huu uendane na takwimu zinaonesha uhitaji upo kwa kiwango gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upungufu wa watumishi katika sekta ya afya, sekta hii inakabiliana na upungufu wa asilimia 49 ya watumishi wa afya katika mwaka a fedha 2016/2017; changamoto hii imekuwa ya muda mrefu hasa maeneo ya vijijini jambo ambalo linapelekea wananchi kukosa huduma na hasa tukilinganisha idadi ya ongezeko la watu nchini. Naishauri Serikali kuhakikisha inaweka mkakati wa haraka wa kuhakikisha inakabiliana na changamoto hii kwani idadi ya watu nayo inaongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu chakula na lishe, tatizo la udumavu nchini ni kubwa kutokana na lishe duni kwa watoto na wajawazito, udumavu huu kwa watoto ambao ndiyo Taifa la kesho maana yake tutatengeneza Taifa la udumavu. Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na REPOA takribani watoto milioni 2.4 wana udumavu; takwimu hii ni kubwa na watoto hawa wengi ni wale walio katika kaya maskini za vijijini. Hivyo basi, Serikali ituambie ina mkakati gani wa kuiwezesha Taasisi ya Chakula na Lishe kifedha na kuweka mikakati ya haraka ya kukabiliana na hali hii ya lishe duni unaosababisha udumavu kwa watoto hapa chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uzazi wa mpango, uwekezaji wa Serikali katika mpango wa uzazi ni jambo la muhimu sana kwani jambo hili limekuwa haliwekewi fedha za kutosha, umuhimu na uhusiano wa mpango wa uzazi na mkakati wa kupunguza vifo vya wanawake wajawazito; uzazi vina mahusiano ya karibu, hata hivyo kukiwepo na uzazi wa mpango ndivyo ambavyo tunaweza kupanga mipango bora ya maendeleo. Nashauri Serikali ihakikishe upatikanaji wa madawa, vifaa vya uzazi wa mpango katika maeneo yote ya utoaji wa huduma ya afya nchini. Serikali iongeze bajeti na kutoa fedha zilizoainishwa za fungu hili. Pia kuwa na huduma na vituo vya afya ya uzazi kwa vijana nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu pensheni kwa wazee; wazee wa nchi hii wamekuwa wakipewa matumaini ya kupatiwa pensheni bila mafanikio yoyote. Je Serikali ina mpango kati wa haraka wa kutoa pensheni kwa wazee nchini?

Mheshimiwa Naibu Spika, uwakilishi na usawa wa kijinsia, kwa mujibu wa takwimu za Employments and Earns Report ya mwaka 2015 nafasi za wanawake walioshika nyadhifa mbalimbali ni asilimia 15 tu ya idadi ya waajiri, wateuliwa na wachaguliwa wote nchini. Idadi hii ni ndogo sana. Hivyo basi Wizara iwajibike kuona ongezeko la usawa wa kijinsia katika nafasi mbalimbali unaongezeka zaidi, nawasilisha
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, uhifadhi wa Ziwa Manyara; ziwa hili ni miongoni mwa maeneo ya utalii hapa nchini kwa watalii wengi kutembelea. Hata hivyo, ziwa hili lipo kwenye hatari ya kupotea/kutoweka kutokana na tope lililojaa ziwani kunakosababishwa na shughuli za kilimo katika maeneo yanayozunguka ziwa. Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka kuokoa Ziwa Manyara ambalo ni kivutio cha utalii hapa nchini?

Mheshimiwa Spika, kuhusu tozo nyingi katika hoteli za kitalii; tunapohitaji sekta ya utalii iendelee kukua na kuongeza pato la Taifa ni muhimu na ni lazima kuhakikisha kunakuwa na mazingira mazuri na rafiki kwa wawekezaji katika sekta hii ya utalii. Hoteli za kitalii zimekuwa zikilipa tozo nyingi sana hivyo kufanya hoteli hizi kuwa na mazingira magumu kuendesha biashara.

Ushauri, Serikali itazame kwa upya tozo hizi ili kuendelea kuwajengea mazingira mazuri wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, TALA ni leseni inayotolewa kwa makampuni ili waweze kuendesha shughuli za utalii. Hata hivyo leseni hii imekuwa ikilipwa na/au kutolewa kwa mtu akiwa na magari matatu kwa kulipa dola 2,000. Hata hivyo, mtu akiwa na magari zaidi ya matatu analazimika kulipa sawa na mwenye magari matatu (kwa kuwa ni takwa la kisheria). Hivyo basi, mtu akiwa na magari 50 au 100 atalipa sawa na mwenye magari matatu. Hapa hakuna usawa na ni unyonyaji kwa watu na kuendelea kuweka mazingira magumu kwa vijana wanaotaka kujiajiri.

Mheshimiwa Spika, ushauri, Serikali itoze leseni hii kwa kila gari, kwa kufanya hivi Serikali itaongeza mapato na kutawapa vijana nafasi/fursa ya kuingia katika sekta ya utalii na kujiajiri.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii, kwa sababu ya muda nitaenda haraka haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ya kilimo inaajiri asilimia 65 ya nguvu kazi ya Taifa; inachangia asilimia 9.9 ya pato la Taifa; inachangia asilimia 65 ya malighafi viwandani na inachangia asilimia 100 ya chakula kinachopatikana hapa nchini. Sekta hii ya kilimo kama ikiwekezwa vizuri itatoa ajira ya kutosha; itaondoa umaskini; tutafikia hicho mnachokitaka kinaitwa Serikali ya viwanda na tutaweza kufikia uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, sekta hii imekuwa haipewi fedha kama inavyotakiwa. Fedha tunazozitenga hapa Bungeni hazifiki kwenye Wizara na kwenda kutekeleza miradi ya maendeleo. Kwa miaka 10 fedha ambayo imepitishwa na Bunge lako ambayo imefika kwenye Wizara hiyo ni asilimia 2 tu. Mwaka huu fedha hizo za miradi ya maendeleo ambazo zinaombwa imekuwa ni pungufu ya asilimia 23 ya bajeti ambayo tulipitisha mwaka 2017/2018. Maana yake ni kwamba sekta hii ya kilimo imeendelea kupuuzwa, kuachwa nyuma na haipewi msisitizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji wa sekta ya kilimo kwa mujibu wa Ripoti ya Benki Kuu ni kama ifuatavyo: Mwaka 2011 ilikua kwa asilimia 1.9; 2012 ilikua kwa asilimia 3.2; 2013 ilikua kwa asilimia 4; 2014 ilikua kwa asilimia 3.4; 2015 ilikua kwa asilimia 3.2; 2016 ilikua kwa asilimia 1.9; 2017 ilikua kwa asilimia 1.3. Serikali ya Awamu ya Nne wakati inaondoka madarakani iliacha sekta ya kilimo ikikua kwa asilimia 3.2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mmeingia madarakani Serikali ya Awamu ya Tano mmejiita Serikali ya Hapa Kazi, Serikali ya Viwanda, mmeweka mikakati ya kufikia uchumi wa kati lakini sekta ya kilimo ambayo inategemewa na asilimia 65 ya Watanzania, ambayo inachangia pato la Taifa imeendelea kushuka na kufikia kiasi cha asilimia 1.3. Kwa wastani maana yake ni kwamba sekta ya kilimo imekua asilimia 1.9 tu. Kila siku mnatuambia uchumi unakua kwa asilimia 7, Watanzania asilimia 65 wanategemea kilimo, halafu uchumi huu wa sekta ya kilimo tu unakua kwa asilimia 1.9 halafu mnataka miujiza mfikie kitu kinachoitwa uchumi wa kati? Haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa nchi hii ni lazima wajue adui yao ni Serikali hii ambayo ina mipango mibovu ya kutoweza kuiwezesha sekta ya kilimo. Asilimia 65 ya Watanzania wanategemea kilimo lakini uwekezaji unaofanywa kwenye sekta hii ni kiasi cha asilimia 0.52 ya bajeti kuu ya Taifa lakini asilimia 5 ya Watanzania ambao wanategemea usafiri wa ndege inapewa kipaumbele ndege unawaacha asilimia 65 ya Watanzania ambao wanategemea kilimo. Huku ni kuwahadaa Watanzania, ni kuwahadaa wakulima, ni kuwadanganya wakulima wa Tanzania. Wakulima wa nchi hii adui yenu ni Serikali hii ya CCM iliyoko madarakani. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia hapa michango ya baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wakilalamikia suala la mahindi kutokuuzwa. Nimeona leo mzigo anashushiwa Mheshimiwa Tizeba pale, hivi tumesahau ni nani alikataza mahindi yasiuzwe. Kauli zikatolewa hapa kwamba mahindi yasiuzwe na Mheshimiwa Waziri Mkuu alisimama hapa akasema hakuna kuuza mazao nje ya nchi. Sasa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanasimama wanampongeza Waziri Mkuu, wanampongeza Rais, wanamshushia mzigo Mheshimiwa Tizeba pale na Mheshimiwa Tizeba ataubeba tu mzigo huu kwa sababu kama huwashauri tunafanyaje.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuongelea kuhusu Jeshi la Zimamoto na Uokoaji. Majukumu ya jeshi hili ni kupambana na majanga ya moto pamoja na kufanya uokoaji pale inapotokea majanga. Jeshi hili umuhimu wake unaonekana zaidi pale panapotokea majanga, hata hivyo umuhimu wake haupewi uzito kutokana na kutopewa fedha za kutosha na vitendea kazi ili waweze kufanikisha majukumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali ihakikishe inalisaidia au inalipatia Jeshi la Zimamoto na Ukoaji fedha za kutosha na vitendea kazi vya kisasa ili utekelezaji wa majukumu uwe na ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, vituo vya polisi nchini. Vituo vya polisi nchini vingi vina uchakavu wa kutisha. Vituo hivi vimekuwa vikihifadhi wahalifu pamoja na uchakavu huo jambo ambalo ni hatarishi kwa usalama. Umuhimu wa kukarabati vituo hivi ni jambo ambalo haliepukiki. Jeshi lipange kimkakati wa ukarabati wa vituo hivi kwa awamu ili kuwa na vitu bora na vinavyokidhi haja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, Jeshi la Magereza. Jeshi hili lina jukumu la kuwahifadhi wafungwa na kutazama mahitaji yao kwa ujumla, lakini majukumu haya hayatekelezwi ipasavyo kwa ufinyu wa bajeti na vitendea kazi ili kufanikisha majukumu yake. Msongamano ni mkubwa katika magereza yetu, magari ya kupeleka wafungwa mahakamani ni machache na mabovu sana. Nashauri Serikali itenge fedha za kutosha ili kukabiliana na upungufu mkubwa uliopo katika hili Jeshi la Magereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, vitambulisho vya uraia. Vitambulisho vya uraia ni haki ya kila Mtanzania kwa kuwa ndicho kinachomtambulisha. Zoezi hili licha ya kushushwa kwenye wilaya zetu limekuwa la kusuasua na kuleta usumbufu na urasimu usiokuwa na ulazima. Wananchi wametakiwa kuchangia fedha ili kupata vitambulisho hivyo. Kwa nini Serikali inachangisha wananchi wakati ni haki ya wananchi kupatiwa vitambulisho. Serikali inawajibika kuwapatia vitambulisho bila vikwazo kwa kuwa Serikali inakusanya kodi ambazo zinapaswa kuwahudumia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasilisha.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hoja iliyoletwa mezani kuhusu Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2018/ 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeeleza vipaumbele vitatu ikiwemo kilimo, viwanda, huduma za jamii kwa maana ya maji, elimu na afya. Mimi nitachangia katika suala la kilimo na elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya CCM toka tumepata uhuru wananchi hii imekuwa na kaulimbiu na mikakati mingi kuhusiana na sekta ya kilimo. Tulikuwa na kaulimbiu na mikakati mingi ikiwemo, Siasa ni Kilimo ya mwaka 1974, Azimio la Arusha la mwaka 1967, Azimio la Iringa mwaka 1974 lakini hata mwaka 2009 tulikuja na Kilimo Kwanza na Serikali ya Awamu ya Nne pia katika Big Results Now, sekta ya kilimo na yenyewe iliongezewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna ambaye anapinga umuhimu wa sekta ya kilimo kwa Watanzania. Nilipochangia Wizara ya Kilimo hapa nilieleza umuhimu wa sekta ya kilimo kwamba inaajiri nguvu kazi asilimia 65 ya Watanzania, inachangia asilimia 30 kwenye pato la Taifa, malighafi viwandani asilimia 65 inatoka sekta ya kilimo na asilimia 100 ya chakula hapa nchini inatoka kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika malengo ya MKUKUTA ya miaka 10, ilijiwekea mkakati wa ukuaji wa sekta ya kilimo angalau kwa asilimia 6 mpaka asilimia 8. Ukuaji wa sekta ya kilimo kwa miaka mitano kuanzia mwaka 2011 mpaka 2015 umekua kwa asilimia 3.4 tu. Hata hivyo, toka Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani, Serikali ya Hapa Kazi, Serikali ambayo inataka kutupeleka kwenye uchumi wa Kati, Serikali inayojiita ya viwanda, ukuaji wa sekta ya kilimo pamoja na umuhimu wake wote umeshuka ukilinganisha na Serikali ya Awamu ya Nne ilivyokuwa madarakani. Ukuaji wa sekta ya kilimo umekua kwa asilimia 1.9 tu toka mwaka 2016 mpaka 2017. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, bajeti ambazo tumekuwa tukizipitisha hapa Bungeni kwenye sekta ya kilimo imekuwa haifiki kwenye Wizara, hazitolewi kwa wakati. Mwaka 2016/2017 tulipitisha Bungeni hapa shilingi bilioni 100 zilizotolewa ni shilingi bilioni 2 tu fedha za maendeleo ni sawasawa na asilimia 2.2. Mwaka 2017/2018 sekta ya kilimo ilitengewa shilingi bilioni 150 zilizotolewa ni shilingi bilioni 16.5 sawasawa na asilimia 11 na mwaka huu fedha zilizoombwa kwenye sekta ya kilimo kwa maana ya Wizara ya Kilimo zitakazotekeleza miradi ya maendeleo ni shilingi bilioni 98.1. Tunawashangaa sana kila siku Serikali iliyoko madarakani, pamoja na kaulimbiu zenu na mikakati yenu mnayosema kwenye vitabu lakini sekta ya kilimo ambayo tunaitegemea sisi Watanzania tulio wengi, mmeendelea kutoipa kipaumbele na kutoona umuhimu wa sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukifanya uwiano kati ya bajeti kuu ya Serikali na sekta ya kilimo, mwaka 2016/2017 uwiano kati ya bajeti kuu na sekta ya kilimo kama ambavyo mmesaini Maazimio mbalimbali ya Kimataifa ni asilimia 0.93, mwaka 2017/2018 ni asilimia 0.85, mwaka 2018/2019 ni asilimia 0.52 na mwaka huu imeshuka zaidi ukilinganisha na miaka mingine. Sasa tunajiuliza mmesema mtaweka kipaumbele chenu cha kwanza ni sekta ya kilimo lakini sekta hiyo hiyo ya kilimo hamuipi fedha, mmewasahau Watanzania wakulima walio wengi, tutawaaminije? Mbona mmetudanganya miaka mingi sana? Mmekuwa wazuri kwenye maandishi, kwenye vitabu lakini kuja kwenye utekelezaji mmekuwa tofauti kabisa. Kwa kweli nirudie kusema, wakulima wa nchi hii adui yenu namba moja ni Serikai iliyopo madarakani kwa mikakati na sera mbovu ambazo hazitekelezeki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kutuambia kwamba kwenye bajeti hii kipaumbele ni kilimo lakini miaka iliyopita, mavuno ya mwaka juzi, wakulima mbaazi tu imewasumbua mpaka leo, kupata masoko ya wakulima wetu mbaazi ni mtihani, korosho ni mtihani, pamba ni mtihani yaani hakuna ambako afadhali, tumbaku ni mtihani, mahindi imewasumbua mwaka mzima yanawahangaisha mnakataza vibali, mnageuka kwa nyuma mnaruhusu vibali. Kahawa imewasumbua, pamba, mkonge, mazao mchanganyiko hakuna mkulima wa nchi anayelima zao lolote ambaye ana uhakika wa soko. Sasa mnasema kipaumbele ni kilimo mnawahakikishiaje Watanzania wakulima kuwa na uhakika wa masoko? Nini mkakati kwenye bajeti hii kuhakikisha wakulima wana masoko ya kutosha? Tunaomba majibu Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kuhusu sekta ya elimu. Serikali ya Awamu ya Tano mmesema mnatoa elimu bure na Serikali ya Awamu ya Nne iliona kutoa elimu bure ni changamoto, ikaona namna bora ni kusaidiana na wazazi kuhakikisha wanakabiliana na upungufu mbalimbali kwenye sekta ya elimu ikiwemo miundombinu na changamoto nyingi katika shule zetu za msingi na sekondari hapa nchini. Ninyi mmekuja, mmefuta michango, mnasema elimu ni bure, Mheshimiwa Waziri kwenye mambo yako 10 uliyoyataja hapa ya kumsifia Rais Magufuli umeelezea suala la elimu bure, nataka nikwambie elimu bure imekuwa na changamoto kubwa, mnaua sekta ya elimu kuliko hata Serikali ya Awamu ya Nne ilivyokuwa madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe takwimu, upungufu wa walimu, shule za msingi, mwaka 2016 upungufu ulikuwa 191,772 mwaka 2017 upungufu umeongezeka umefika 179,291; shule za awali, upungufu wa walimu umekuwa 1,948; shule za sekondari masomo ya hisabati upungufu wa walimu ni 7,000, baiolojia 5,000, kemia 5,000, na fizikia 6,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa miundombinu; upungufu wa maktaba…

T A A R I F A . . .

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, siipokei hiyo taarifa na kitu ambacho nafikiri Serikali mnakosea sana, mnapima mafanikio ya elimu bora na idadi ya uandikishwaji siyo quality na hiki kitu mmekuwa mnakisema siku nyingi. Pia idadi ya wanafunzi wanaondikishwa inawezekana ikaongezeka kwa sababu ya uzao, birth rate nayo inawezekana ikawa inaongezeka, population inaongezeka, sasa mnapimaje hayo? Mheshimiwa Naibu Waziri utapata nafasi baadaye na wewe utasema ya kwako.
(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa maktaba; mwaka 2016 upungufu ulikuwa ni asilimia 88, mwaka 2017 upungufu umekuwa ni asilimia 91. Maana yake badala ya kwenda mbele kupunguza changamoto mbalimbali za kimiundombinu tunarudi nyuma hatua kadhaa haya matatizo yanazidi kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maabara; upungufu wa maabara ya baiolojia ni asilimia 51, fizikia 54 na kemia 53. Upungufu wa madawati ni milioni 1,170,000 na upungufu wa walimu ni 186,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajiuliza, mnatuambia elimu bure, elimu hii siyo bure, mnakwenda kuua Taifa la kesho. Badala tuliandae Taifa la kesho, mnajua umuhimu wa elimu ni kuandaa rasilimali watu, kuliandaa Taifa, tuwe na wataalam na wajuzi wa kutosha, tuandae mazingira ya kufikia haya, tunatengeneza mazingira mabovu ya kuwa na elimu mbovu ya kuiangamiza nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia ripoti ya LAAC na mimi pia ni mjumbe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya mwaka 1998 na mwaka 2008 ilifanyika reforms kubwa sana kwenye Local Government na ilitumia fedha nyingi. Reforms hizo zilielekeza kuwajengea uwezo watumishi kwa maana ya Mkurugenzi na timu yake na menejimenti kwa ujumla lakini pia reformshizo ziliwajengea uwezo Madiwani katika kusimamia fedha za Halmashauri zinazoletwa katika Halmashauri zao na reforms hizi zilitumia fedha nyingi kama nilivyoeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano ilipoingia madarakani kwa kweli imeonesha kabisa kutokuzithamini Local Government kwanza kwa uteuzi tu uliofanyika wa ma- DED tumeona ma-DED walioteuliwa kwa kiwango kikubwa wengi hawana uwezo, hawakutoka kwenye mfumo wa Local Government. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma utaratibu uliokuwa unatumika kutokana na hizo reformszilizofanyika, Mkurugenzi alikuwa anateuliwa ni mtumishi wa Serikali za Mitaa ambaye amehudumu kwa kipindi kisichozidi miaka mitano anaenda kuteuliwa kushika hiyo nafasi. Hii maana yake ni kwamba alitakiwa awe anazielewa Serikali za Mitaa, ajue kusimamia fedha vizuri, aielewe Serikali za Mitaa kwa ufanisi zaidi, lakini sasa hivi watendaji walioteuliwa kwa kweli hawana uwezo wowote.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya ndiyo yanayosababisha tunaona Local Government leo hata miradi kwanza miradi yenyewe inayotekelezwa vipaumbele vinavyowekwa havifikiwi na wala havifanyiki kwa sababu ya upungufu huo. Pia reforms zile zilijenga uwezo kwa Madiwani, leo Madiwani wetu kwanza hata baadhi ya Halmashauri vikao havikai, hakuna fedha. vikao havifanyiki, Kamati za Fedha hazisimamii ipasavyo hata hizo fedha kidogo zinazopelekwa kwenye Local Government. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nadhani tufike mahali kama nchi kama utawala wa awamu fulani unafanya mambo wa kadha wa kadha. Mfano, kama tulifanya reforms kwenye tawala zilizopita huko nyuma, utawala unaokuja hauna budi kurithi na kuhakikisha inaendeleza yale ambayo yaliendelezwa na utawala uliopita na sio kupindisha. Nadhani uzalendo wa nchi hii ni pamoja na kuyaenzi na kuyatekeleza yalifanyika kwenye awamu zilizopita na kuendeleza na si kuharibu ama kufanya ambavyo haitakiwi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeongea toka tunaanza Bunge hili na sasa tunaelekea ukomo wa Bunge hili. Tumeeleza jinsi ambavyo Serikali za Mitaa zimenyang’anywa mapato ya uhakika ambayo kwa kiwango kikubwa ndio yalikuwa yanasaidia kuwepo na uhai wa Serikali za Mitaa.

Leo wamenyang’anya vyanzo vya uhakika, mambo hayaendi kwenye Serikali za Mitaa, tutaendelea kuwataka Serikali kuhakikisha kwanza vyanzo vya uhakika kwenye Local Government vinarudishwa, waziachie Halmashauri zikusanye mapato/hizo fedha ili iweze kuendeleza miradi katika maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni hiki kitu kinachoitwa force account; Serikali inaisemea sana na kuipigia chapuo, lakini mimi naona kutakuwa kuna shida kubwa sana mbeleni. Hizi force account miradi inayotekelezwa kwaforce account inaenda kutekelezwa kwa kiwango kikubwa na hao mafundi ambao watateuliwa kwa utaratibu unaokuwepo lakini hatuangalii ubora wa majengo yanayojengwa kwa force account. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawataka wasimamizi kwa maana ya Mainjinia wa Wilaya wakasimamie lakini tuna mainjinia wangapi kwenye wilaya moja wakasimamie miradi hii kuangalia ubora wa majengo yanayojengwa? Mainjinia wenyewe hawatoshi, utakuta kwenye wilaya moja labda kuna miradi minne ama mitano inayojengwa kwa force account halafu unataka injinia mmoja kwenye Halmashauri kwa sababu pia tuna upungufu mkubwa sana kwenye Halmashauri, unataka injinia huyohuyo mmoja akasimamie, hivi ufanisi wa miradi hii uko wapi?.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapokwenda mbele watakuja kuona miradi ya force account majengo yanaanguka tu hovyo hovyo kwa sababu hayajajengwa kitaalam, hayana usimamizi wa kila siku, tunawaachia hao mafundi sanifu ambao kwa kweli hawakidhi vigezo wanaenda wanazitazama hatuwaachii mainjinia, kwanza hatuna lakini haipati usimamizi wa kutosha kuhakikisha kwamba miradi hii kwa kweli inasimamiwa inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la miradi ya mikakati. Kuna fedha nyingi sana zinakopwa kwa ajili ya miradi ya mkakati. Mfano hapa Dodoma…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umeisha Mheshimiwa, zilikuwa dakika tano, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie katika hoja iliyoko mbele yetu kuhusiana na Mpango wa Maendeleo wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ni kama desturi au taratibu zinatutaka tupitishe Mipango hii na mara nyingi imekuwa ni Mipango mizuri sana kwenye maandishi na imekuwa ni Mipango mingi kwa mara moja lakini ukija kwenye utekelezaji ndipo ambapo kunakuwa na changamoto kubwa. Utekelezaji umekuwa ni hafifu kwa sababu kwanza tumekuwa na mipango mingi ndani ya mwaka mmoja wakati tunaambiwa hako kasungura tunakokakusanya nako ni kadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni bora tuwe na Mipango michache ambayo inahusiana moja kwa moja na maisha ya mwananchi wa kawaida, tukaitekeleza kwa ufanisi, tukamsaidia yule mwananchi wa chini kabisa maskini. Tukipitisha mipango tukaenda kupitisha na bajeti maana yake fedha zitolewe na bajeti hiyo iweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, tunapitisha mipango mbalimbali kwenye sekta zote muhimu zinazomgusa Mtanzania mfano ya kilimo, maji, viwanda, afya, yote kwa namna moja au nyingine inamgusa mtanania wa chini kabisa. Hata hivyo, tukipitisha Mipango hii ukija kwenye kuangalia namna gani bajeti zinapitishwa kwenye Wizara hizi haiendani kabisa na kile ambacho tumekipitisha. Fedha hazitolewi kwa wakati, wakati mwingine hata kikitolewa hicho kidogo kinafika kwa kuchelewa maana yake kile tulichokipitisha basi kinakuwa ni kama hakuna kwa sababu hakuna matokeo ambayo yanafikiwa kulingana na kile ambacho tumekipitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la mfumuko wa bei, ukisoma Mpango hapa unaeleza kabisa kwamba mfumuko wa bei Serikali imeendelea kudhibiti. Uhalisia sidhani kama iko hivyo, inawezekana imedhibitiwa kwenye makaratasi lakini tukitoka nje ya jengo hili huo mfumuko wa bei unaosemwa haujadhibitiwa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia Desemba mwaka jana mpaka leo hii January tunapoongea kuna mfumuko mkubwa sana wa bei ya bidhaa. Mfano, unga wa ngano wa kilo 50 ilikuwa inanunuliwa kwa Sh.60,000 leo unanunuliwa kwa shilingi 69,000. Unaenda kwenye mafuta ya kula ya lita 20, yalikuwa yananunuliwa kwa shilingi 52,000 leo yananunuliwa kwa shilingi 82,000. Ukienda kwenye bidhaa za ujenzi, vivyo hivyo, bati zimepanda bei, saruji ndiyo usiseme. Saruji sio tu kupanda bei, yaani saruji imekuwa bidhaa adimu ndani ya nchi hii na tuna viwanda. Saruji ilikuwa inanunuliwa kati ya shilingi 13,000 au shilingi 14,000 leo unaitafuta kwa shilingi 17,000 mpaka shilingi 28,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukisoma Mpango, Hali ya Uchumi wanakwambia mambo ni mazuri, Serikali ya wanyonge inasema hakuna mfumuko wa bei mambo yako sawasawa. Sasa, mambo kweli yako sawasawa kwenye makaratasi lakini hayako sawasawa tukitoka nje ya hapa. Bati za geji 8 zilikuwa zinanunuliwa kwa Sh.62,000 leo zinafika Sh.70,000 na zaidi. Nadhani yale mnayoyanena kwenye makaratasi basi yanenwe kwa vitendo huko nje tunakotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la mfumuko wa bei nadhani lipatiwe ufumbuzi sasa hivi halisubiri bajeti. Mtuambie, Watanzania huko nje wanataabika, mambo ni magumu, kila kitu kimepanda bei hatuelewi ni kwa nini kimepanda bei na bidhaa nyingine hazipatikani kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ambayo napenda kuichangia ni kuhusu wafanyabiashara. Wafanyabiashara wa nchi hii imekuwa kama ni ule mchezo wa paka na panya. Ni mchezo wa kuviziana, wa kutafutana. Leo wafanyabiashara wa nchi hii wako wengine ambao wanaamua kufunga biashara kwa sababu mazingira ya ufanyaji wa biashara siyo rafiki hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hapa Dodoma hivi tunavyoongea kuna wafanyabiashara wengi tu wameshaandikiwa barua na TRA; wengine wanataka kufungiwa akaunti na wengine wanaanza kufikiriwa kupelekewa hiyo task force ya kuangaliwa kodi ya miaka mitatu nyuma. Kuna wafanyabiashara kule Karatu wamepelekewa hizo task force zinawachunguza eti wanachunguzwa mapato yao kwa miaka mitatu nyuma yalikuwaje wakati huyu mtu analipa kodi yake kila mwaka hajawahi kukwepesha kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunaambiwa mashamba hayatozwi kodi, Karatu kule kuna wafanyabishara kwenye Bonde la Eyasi wanalima vitunguu, wote wameambiwa wanapelekewa hiyo task force inachunguza kwa miaka mitatu namna gani wanalima, mapato yao ni nini, wana wafanyakazi kiasi gani, wanatakiwa kulipa nini na kwa nini hawajalipa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Cecilia Paresso.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, wote wanalima mashamba ya vitunguu, lini tumeanza tena kutoza kodi mpaka mashamba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ushauri wangu kwa Serikali.

SPIKA: Muda wako umeisha.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, samahani kidogo tu nimalizie, ili uweze kuongeza mapato ni kuwatengenezea wafanyabiashara mazingira rafiki na unapunguza kodi, ndivyo ambavyo utapata kodi nyingi. Ukiongeza kodi unafukuza na kufunga biashara. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu. Na kwasababu, muda ni mfupi basi nitachangia katika jambo moja na kama itatosha basi, nitaenda kwenye jambo la pili. Ninapenda kuishauri Serikali katika suala zima la wafanyabiashara wetu hapa nchini. Tunatambua umuhimu wa wafanyabiashara na lazima Serikali ilione hilo kwasababu hawa wafanyabiashara wakifanya biashara katika mazingira rafiki, kwa maana ya mazingira ya amani yenye kutenda haki ndivyo ambavyo watalipa kodi na wakilipa kodi ndivyo ambavyo hii mipango yote tunayoiongea humu Bungeni inaweza kwenda kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia huko nyuma jinsi ambavyo wafanyabiashara wengi wamepitia kadhia mbalimbali. Na tunamshukuru Mheshimiwa Mama Samia angalao ameliona hilo na ameanza kulisemea kuhusiana na changamoto ambazo wafanyabiashara wanazipata. Sasa pamoja na Mheshimiwa Mama Samia kulisemea, tunaomba watendaji walioko chini wanaosimamiwa na Mheshimiwa Rais haya anayoyasema yaende kutekelezwa kwa vitendo kwa kuhakikisha wafanyabiashara wanatendewa haki, wanafanyiwa makadirio ya kodi ambayo ni rafiki na yanalipika. Lakini kama haitoshi wanahakikisha kwamba, sheria, taratibu na kanuni zilizoko zinatekelezwa, ili mwisho wa siku huyu mfanyabiashara alipe ile kodi ambayo anastahili kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho ni muhimu kitazamwe na Serikali ni lazima kuwepo na viwango vya kodi ambavyo ni reasonable, ili mfanyabiashara aweze kulipa, lakini pia tusifikirie kuweka wigo makadirio makubwa ya kodi, tukipunguza makadirio ya kodi tutawafanya wafanyabiashara wengi walipe kodi na kodi itaongezeka. Ukifanya kodi kuwa kubwa maana yake utawapunguza wafanyabiashara, lakini ukipunguza utaongeza na wengine wengi watalipa kodi bila kusumbuana, bila bughudha yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Awamu ya Tano kulikuwa kuna task force ziliundwa, na hizi task force zimewafuata baadhi ya wafanyabiashara katika maeneo mbalimbali ndani ya nchi zikawafanyia uhakiki wa hesabu kwa miaka mitatu, mitano ya nyuma iliyopita. Tunatambua kuna tamko limeshatoka, lakini tunaomba hilo tamko liwe kwa vitendo, kuna wafanyabiashara bado leo wanaambiwa wana ma- document wanaambiwa walipe. Hawa wafanyabiashara walishalipa kodi kwa utaratibu unaotakiwa wakapelekewa task force wakaanza tena kukagua kwa upya wanaambiwa tena walipe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Serikali ilifanye hili kwa vitendo kwasababu, nimeona Waziri wa fedha amelisema kupitia vyombo vya habari, lakini hawa watu watapataje comfort kama hawana hata document kutoka TRA kwamba, zile hesabu zako za nyuma sasa hatuzifanyii kazi tena tunatizama mbele. Kwa hiyo, niishauri Serikali wafanyabiashara wote ambao wamepitia adha hii tunaomba muwape comfort ama uhakika wa hayo kwa kuwaandikia barua ili wawe na amani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, kati ya mwaka 2019 na mwaka 2020 wafanyabiashara wa maduka ya kubadilishia fedha katika Mkoa wa Arusha na maeneo mengine nchini hao nao ni kati ya watu ambao wameumizwa kwa kiwango kikubwa na hawajui hatima yao. walipelekewa task force wakanyang’anywa fedha zao tena ni unyang’anyi, wakachukua fedha zote zikaenda Benki Kuu, wakiuliza sababu hakuna sababu. Na tukumbuke utaratibu unasemaje, mfanyabiashara yeyote anapotaka kuanzisha biashara yoyote lazima apate TIN Number, apate leseni ya biashara, kabla ya leseni ya biashara maana yake atapata tax clearance. Maana yeke huyu hana shida yoyote anapewa hiyo leseni ya kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hawa wafanyabiashara wa maduka ya kubadilishia fedha katika Mkoa wa Arusha na maeneo mengine walikuwa wamefuata procedure zote za kuanzisha biashara, wakawa wana leseni zote tena leseni Hai, wanalipa kodi inavyotakiwa, lakini ikaja task force kwa bunduki, kwa magari mengine ambayo hayajulikani sijui namba zipi, wakakwapua fedha zao zikarudishwa BOT. Tunaomba kufahamu nini hatima ya wafanyabiashara hawa? Kwa sababu, walikuwa wanaendesha biashara kihalali kabisa, mmewachukulia fedha zao; Serikali inaema nini kuhusiana na hawa watu ambao mmewanyang’anya fedha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama haitoshi hata wako wengine ambao wamepoteza maisha kwa matukio ya namna hii. Mtu unamnyang’anya karibia bilioni kumi, ishirini na anafanya biashara kihalali matokeo yake mtu anafariki kwa pressure, kwa mambo kama haya. Na hawa mnawafidia nini kwasababu wana familia wana watu waliowaacha kwa hiyo, ni vema mkalitizama hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama hiyo haitoshi kuna wafanyabiashara wengine wapo magereza leo kwa kubambikiziwa kesi za uhujumu uchumi, kukwepa kulipa kodi wakati wanalipa kodi, hatujasikia nao hawa mnawafanyia nini? Tunatamani kuona yale ambayo Mheshimiwa Mama Samia ameyanena basi tuyaone kwa vitendo kwa watu kama hao ambao wameonewa kwa namna moja ama nyingine haki itendeke, watoke wawe huru, kama kuna sheria ambazo tunahitaji kuzifanyia marekebisho Serikali mzilete hapa Bungeni tufanye marekebisho Watanzania wafanyabiashara wafanye biashara kwa uhuru, haki na amani lakini wakijua wajibu wao ni kulipa kodi ambayo inaweza ikalipika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu ya Wizara ya TAMISEMI.

Kwanza nianze kwa kutoa pole kwa familia mojawapo katika Kata ninayoishi, Kata Qurus Karatu kwa kuondokewa na mtoto mdogo wa Darasa la Kwanza aliyefariki leo asubuhi wakati anaenda shuleni akavamiwa na fisi, akafiriki, nawapa pole sana.

Mheshimiwa Spika, hii ni ujumbe kwa Serikali kwamba ipo haja ya kuangalia hizi shule zetu za msingi, zijengwe katika mazingira karibu na jamii ya maeneo yale. Vile vile muda wa kwenda shuleni asubuhi kwa hawa watoto wadogo wa Darasa la Kwanza na la Pili kwa sababu ya umri wao kwa kweli sidhani kama ile asubuhi mapema lazima wawe wanafika shuleni ili kuwaweka katika mazingira salama zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, inaweza ikafikiriwa kuwa reviewed hawa watoto wadogo wa Darasa la Kwanza wanaoenda shuleni asubuhi wakawa wanaingia hata mchana ili kuwaweka katika mazingira salama zaidi wanapoenda shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo, nichangie katika mambo matatu yafuatayo: kwanza, ni kuhusiana na uhaba wa nyumba za walimu katika shule zetu za msingi na sekondari. Ili tuweze kutoa elimu katika ubora na viwango vinavyotakiwa, pamoja na uwepo wa walimu, pia ni kuhakikisha tunakuwao na miundombinu rafiki yenye kutosheleza ili tuweze kutoa elimu inayotakiwa kwa watoto wetu na kupata ubora ambao tunaoutarajia kama Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kitabu cha takwimu cha elimu Tanzania, uhaba wa nyumba za Walimu katika shule zetu za msingi, tuna upungufu wa nyumba za Walimu 204,141na kwa shule za sekondari tuna upungufu wa nyumba za Walimu 67,699; jumla ya upungufu nyumba za Walimu katika shule zetu za msingi na sekondari kama nchi tuna upungufu wa nyumba 271,874. Sasa ukiangalia takwimu hizi na ukiangalia kilichotengwa kwa mwaka huu fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Walimu maana yake Serikali inatarajia kujenga nyumba za Walimu 300 tu katika upungufu wa nyumba 271,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ukifanya mahesabu, maana yake kila mwaka kama tutakuwa tunajenga 300, wakati tuna upungufu wa 200,000 plus, maana yake tunahitaji miaka 906 ili kukamilisha ujenzi wa nyumba hizi za Walimu hapa nchini. Sasa ni vyema Serikali ikalitazama hili, kama kweli tunataka elimu iliyo bora na kama tuna upungufu wa kiwango hiki, basi waje na mikakati thabiti ya kuona namna gani tunaondokana na upungufu wa nyumba za Walimu hapa nchini katika shule zetu zote za msingi na za sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia pia uhaba wa madarasa; uhaba wa madarasa unapelekea wanafunzi wengi kutokupata nafasi za kwenda kuendelea, mfano wakimaliza darasa la saba wanataka kwend form one mara nyingi tumeshuhudia ikifika ule wakati ufaulu ukiongezeka Wakurugenzi, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya wanakimbizana, yaani tunafanya zimamoto kujenga madarasa ili wanafunzi waliofaulu wote waweze kwenda shuleni. Sasa takwimu zipo zinaonesha kabisa wazi, mfano, mwaka 2018 wanafunzi waliokosa nafasi ya kwenda kidato cha kwanza kwa sababu ya uhaba wa madarasa ni 134,000; mwaka 2019 imepungua kidogo imekwenda 21,000; mwaka 2020 waliokosa nafasi ni wanafunzi 59,700.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu, kuna Sera ya Elimu bure, hii sera ndio inakuja kuleta matokeo haya ambayo tunayaona, kwamba ufaulu ukiongezeka maana yakje wanapokwenda huko form one wanakosa madarasa, hili linajulikana. Sasa kwa nini Serikali isiweke pia mkakati wa kuhakikisha upungufu wa madarasa unakwisha, wanafunzi wote waliofaulu wanakwenda shule. Takwimu zinaonesha shule ya msingi, upungufu ni madarasa 82,200; shule za sekondari upungufu ni madarasa 4,647. Huu upungufu ni mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunapojadili suala la elimu na tukitaka kweli tutoe elimu iliyo bora kwa wanafunzi wetu, tukitaka nchi yetu itoe product nzuri kwenye sekta ya elimu hatuna budi kuwekeza kuhakikisha nyumba za Walimu na madarasa yanakuwepo na kuhakikisha kwamba wanafunzi waliofaulu wanakwenda shule na isije ikatokea sababu hawaendi shule eti kwa sababu tu hakuna madarasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie hoja ya mwisho ambayo nimejikita kuzungumzia leo, ni suala la udhibiti ubora katika Idara ya Udhibiti Ubora...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na niweze...

NAIBU SPIKA: Utafatiwa na Mheshimiwa Mwanaidi Hamis.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze jambo la kwanza kuhusiana na kampeni ya usafi wa mazingira kitaifa, kampeni hii ililkuwa inafanywa na wadau muhimu ambao walikuwa na slogan yao ya nyumba ni choo. Mradi huu uliendeshwa kwa kuijenga jamii kuelewa namna bora ya kuwa na vyoo bora lakini kunawa mikono na kuhakikisha kwamba wanakuwa na vyoo vinavyotumika kwenye kila kaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kampeni hii ilikuwa ina ufanisi mkubwa sana kwasababu imezunguka kwenye mikoa 18 na matokeo yake ni kuongezeka kwa kaya zenye vyoo bora kutoka asilimia 39 mwaka 2017 hadi asilimia 67 mwaka 2021. Haya ni mafanikio makubwa, lakini pia kampeni hii inasaidia mwisho wa siku kuibadili jamii kitabia na kimienendo lakini inasaidia kuweka kinga kwenye jamii ili kusiwepo na magonjwa mbalimbali ya maambukizi ambayo yanatokana na ukosefu wa vyoo katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi ni vyema Wizara natambua mradi huu unaisha na mradi huu ulikuwa funded na Wizara basi ni vema Wizara ikaendelea kuwekeza kwenye kampeni hii ambayo itaendelea kuisaidia jamii kujiandaa kukabiliana na magonjwa mbalimbali lakini kuwa na vyoo bora kunawa mikono kwa maji tiririka na sabuni hii mwisho wa siku inasaidia hata katika magonjwa mbalimbali ya milipuko kama Corona na mengine ambayo hatujui kama yatakuja au hayaji kuisaidia jamii kuiandaa katika ustawi bora Zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili kuna hii dawa ya Phyt Exponent, ninaushahidi imesaidia kwa mtu ambaye alikuwa anaumwa corona lakini wako wengine ambao walikuwa wanaumwa kansa imeonyesha matokeo bora na mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa dawa hii ni ghali na upatikanaji wake kwa watu wa kawaida siyo rahisi inauzwa 150,000 sababu za kuuzwa 150,000 kwasababu haijasajiliwa kama dawa tunaiomba Wizara kwasababu imeshathibitishwa na Mkemia Mkuu wa Serikali, na imeshaonyesha matokeo na hata hivyo mtu anapougua mwisho wa siku imani ya mtu kutokana na anachokitumia kinasaidia kuponya, watu wanaimani na hii basi tunaomba Wizara isajili hii diet Supplement ili iweze kupatikana kwa urahisi na kwa unafuu na iweze kusaidia jamii yetu kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu, ni Idara ya Maendeleo ya Jamii Idara hii ya Maendeleo ya Jamii ina watu wa Ustawi wa Jamii na Watu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii. Watu wa Ustawi wa Jamii ni muhimu sana kwenye jamii yetu na watu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii ni muhimu sana kwenye jamii yetu kwasababu inaiandaa jamii kukabiliana na changamoto mbalimbali lakini inaleta chachu ya maendeleo katika jamii kwa kuihamasisha jamii. Lakini Idara hii sina hakika kama Wizara na Serikali kwa ujumla mnaona umuhimu wa Idara hii na kuhakikisha kwamba kunakuwa na rasilimali watu wa kutosha katika idara hii ili isaidie jamii kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mahitaji ya watu ustawi wa jamii ni 22,000 lakini walioajiriwa ni watu 744 kwa hiyo kuna ajira iliyotolewa walioko kazini Maafisa Ustawi wa Jamii ni asilimia 3.2 ya uhitaji wote wa nchi nzima hiki ni kiwango kidogo kabisa. Ni vema Serikali ikaweka umuhimu kwa kuhakikisha tunaajiri maafisa ustawi wa jamii wa kutosha hawa maafisa ustawi wa jamii wa kutosha wakipatikana ndivyo ambavyo tutaijenga jamiii yetu kimaadili tutachochea maendeleo, tutahakikisha ukatili tunaouongelea kila siku ukatili wa watoto, ukatili wa kijinsia, mambo mengi yanayoendelea katika jamii yetu kama tuna watu kama hawa wa kutosha kwenye halmashauri zetu tutahakikisha tunakuwa na jamii yenye ustawi yenye amani yenye kuwa na maendeleo ambayo tunayahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie hoja yangu ya mwisho upungufu wa watumishi katika sekta ya afya, takwimu zinaonyesha kuna upungufu wa watumishi wa afya ni asilimia 53 sasa kama tutakuwa tunajivunia tunajenga zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya tunaimarisha hospitali za kanda tutabakiwa na majengo yasiyokuwa na watumishi wa kutoa huduma muhimu za afya kwa watu wetu. Tunataka Serikali muwe na mpango sambamba mpango wa kujenga zahanati zetu vituo vya afya na hospitali za wilaya uendane na mpango wa kukajiri watumishi kuhakikisha watumishi wanapatikana wakutosha watanzania wanatamani kupata huduma iliyobora ya kutosheleza na ya uhakika kwa kuwa na watumishi wa afya wakutosha ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo. Nianze kwa kumpongeza Waziri na Naibu Waziri kwa jinsi ambavyo mlipambana vya kutosha wakati tumepata baa la nzige. Kwa kweli hongereni mlifanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna ambaye hatambui umuhimu wa kilimo hapa nchini na sote tunatambua jinsi gani ambavyo kilimo kinachangia kwenye uchumi wetu au kwenye pato la Taifa kwa maana asilimia 26 ya pato letu la Taifa linatokana na sekta ya kilimo, kinatoa ajira kwa asilimia 58 lakini mauzo ya bidhaa za nje kwa asilimia 30 na pia sekta ya kilimo inachangia asilimia 65 ya malighafi viwandani.

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano uliweka kipimo kwamba kilimo kiweze kukua kwa asilimia 7.6 lakini hadi leo kilimo hiki kimekuwa kwa asilimia 4.9 Sasa tunaweza kujiuliza kwamba kama tunajiwekea mipango au vipimo fulani vya kutupima kama nchi na hatuvifikii maana yake kuna visababishi vingi ambavyo vinasababisha hicho ambacho tunakiweka tusikifikie.

Mheshimiwa Spika, mojawapo kwanza kilimo hakipati uwekezaji wa kutosha. Kama nchi sina hakika kama tumeona kilimo pamoja na haya nilioyataja huko juu namna gani kinachangia uchumi wa nchi lakini sina hakika kama Serikali mmeona umuhimu wa kuwekeza vya kutosha kwenye kilimo ambacho kinawasaidia Watanzania wengi sana karibia asilimia 80. Hivyo basi ni muhimu sana mkaona umuhimu wa kuwekeza vya kutosha kwenye kilimo. Kama ambavyo tunafanya jitihada kubwa ya kuwekeza kwenye miundombinu kwa maana ya labda Wizara ya Ujenzi, barabara, Siegler’s, SGR na kila kitu, vivyohivyo tufikirie namna gani ya kuwekeza vya kutosha kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiwekeza vya kutosha kwenye sekta ya kilimo maana yake hata hawa vijana wetu walio nje wengi huko hawana ajira wanamaliza vyuo, tukifanya mazingira mazuri na watu wakapenda kilimo na watu wakaona kilimo si tu cha kupanda mahindi kwa maana ya mahitaji ya chakula lakini wakafikiri kwamba nitapanda mahindi lakini pia itakuwa ni sehemu ya biashara na kuniingizia kipato. Maana tunahitaji pia kubadilisha mitizamo ya watu kwa kuwawezesha kwamba ninalima kilimo kama biashara na akiba nitakayopata nyingine itakuwa kama chakula. Kwa hiyo, tunahitaji sana kuwa na mbinu hizo za kubadilisha mfumo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia mchawi mwingine mkubwa wa kilimo chetu ni fedha tunazoidhinisha hapa Bungeni za miradi ya maendeleo, haziendi kama inavyotakiwa. Tukitafuta uchawi ni nini? Nadhani uchawi mkubwa uko hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano, mwaka 2017/2018, tuliidhinisha shilingi bilioni 150 kwenye fedha za maendeleo tu, zilizokwenda ni shilingi bilioni 27. Mwaka 2018/2019, tuliidhinisha shilingi bilioni 98, zilizoenda ni shilingi bilioni 46; mwaka 2019/2020 tuliidhinisha shilingi bilioni 143, zilizoenda ni shilingi bilioni 46. Mwaka huu ambao bado hatujaumaliza, lakini mpaka Aprili, tuliidhinisha shilingi bilioni 150 lakini mpaka Aprili zilizotoka ni shilingi bilioni 68. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tusitegemee muujiza wa kuikomboa sekta ya kilimo kama hata hiki kidogo tunachokitenga hakiendi. Ukiangalia hapa, maana yake hata asilimia 50 ya fedha tulizotenga kwenye miradi ya maendeleo kwa maana ya kilimo, hazijawahi kutoka kwa miaka hii niliyoitaja. Ndiyo maana nasema upo umuhimu wa Serikali kuona kwamba tunawekeza vya kutosha kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hebu tuiombe na kuishauri Serikali kwamba safari hii hiki ambacho tutakipitisha hapa kiende kwa asilimia angalau 80. Halafu tujipime kwamba hicho tutakachokipeleka: Je, kweli kitakwenda kufanya yale tunayoyakusudia na kuleta mapinduzi ya kilimo?

Mheshimiwa Spika, huko nyuma tulikuwa na slogans nyingi za kilimo, wakati wa Serikali ya Awamu ya Nne pia kilimo kiliingia kwenye Big Results Now, Kilimo Kwanza, mambo mengi sana. Ni vyema hizo slogans tunazoziweka na hiyo mikakati tunayoiweka tuitekeleze kwa Serikali kutoa fedha zinazotakiwa, zilizoidhinishwa hapa Bungeni zitoke zote kama ambavyo inatakiwa. Hilo ni muhimu sana. Hapa tutakuwa tumeondokana na uchawi wa sekta ya kilimo kwa ujumla, angalau tutakuwa tumepunguza. Kwa hiyo, ni muhimu sana Serikali ikatazama hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi, kwa mujibu wa report ya CAG, ameonesha mambo mengi sana ambayo ni changamoto au ni madhaifu kwenye sekta ya kilimo. Ameonesha mfano mmojawapo, kwamba wakulima hawana ujuzi wa matumizi ya mbegu, mbolea na viuatilifu. Sasa haya ni mambo ambayo Wizara mnaweza kuyafanya yakatekelezeka, mkulima huyu akapata ujuzi, akajua matumizi ya mbegu bora, akajua matumizi ya mbolea sahihi kulingana na ardhi yake, anatakiwa atumie mbolea gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii itakwenda sambamba na kuangalia yale maabara ya kupima udongo, kwamba hapa udongo huu nikilima naweza kutumia mbolea ya aina gani? Ifike mpaka wilayani, tusiweke tu hivi vituo kwenye centre za mikoa, ni ngumu kwa mwananchi kufika, lakini tukiweka mpaka centre za halmashauri zetu kwa Maafisa Ugani kule chini, maana yake tutakuwa tumemsaidia mwananchi kwa kumpa ujuzi kujua kwamba udongo wangu hapa ninapaswa kutumia mbolea ya aina gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo linguine, CAG ameonyesha kwamba, “kuna usambazaji wa pembejeo usiokuwa na ubora. Hii ni kutokana na kwamba Serikali mmeshindwa kudhibiti.” Haya siyo maneno yangu, ni maneno ya report ya CAG ameeleza. Sasa ni mambo ambayo yako chini ya uwezo wenu Wizara kuhakikisha mnadhibiti. Bila shaka hili hata kama linahitaji fedha, siyo nyingi sana. Ila tunaweza kuona namna gani tunadhibiti haya ili kuhakikisha kile tunachokusudia katika usambazaji wa pembejeo, basi ufanyike kwa kadri ambavyo inatakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo linguine, CAG amesema kwamba kwa mwaka 2016/2017 mpaka 2019/2020, ni asilimia 39 tu ya ugavi wa pembejeo ulifanyika kwenye mbegu, mbolea na viuatilifu. Sasa tuone kwamba kama tunaweza kununua kwa asilimia 39 tu; na inawezekana hii ni kwa sababu ya ufinyu wa bajeti, tusitegemee muujiza. Kama hatufiki hata asilimia 50 ya ununuzi wa hivi vitu ili viweze kumfikia mkulima, tusitegemee mkulima aweze kusaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri sana Serikali na Wizara, CAG ameeleza mambo mengi sana, mkifanyia kazi haya ambayo ameeleza kama ni changamoto, bila shaka tunaweza kuvuka hatua moja mbele kuhusiana na sekta ya kilimo kumkomboa mwananchi na mkulima wa Tanzania kuhakikisha kwamba kilimo chetu kinakuwa na faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema kwamba tunahitaji pia kufanya Watanzania wakipende kilimo. Vijana wetu wakimaliza shule wasifikirie tu kazi ni kwenda ofisini, waone pia kilimo ni kazi ambayo inaweza kumpatia kipato na kuendesha maisha yake kwa Serikali kujenga mazingira mazuri.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nami naungana na Wabunge wenzangu kukupongeza kwa nafasi hiyo ya kuwa Mwenyekiti wa Bunge. Hongera sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita katika mambo yafuatayo: kwanza, sote tunatambua umuhimu wa sekta ya utalii kama nchi, kwa sababu ni sehemu ya kutoa ajira, kuchangia pato la Taifa, kuiingizia nchi fedha za kigeni. Utalii wetu umejikita zaidi kwenye utalii wa wanyamapori. Hivyo basi, bado tuna fursa nyingine nyingi za kupanua zaidi utalii wetu ili uendelee kuwa na manufaa kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina budi kuhakikisha utalii wetu unakuwa endelevu kwa kuendelea kutunza maeneo yetu ya utalii, kuvihifadhi, kuhakikisha haviharibiwi, kuhakikisha kile ambacho kinawavutia wageni kuja na kutupatia faida kama nchi, basi vinatunzwa kwa nguvu zote na kuhakikisha vinakuwa endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna athari za kutoweka hatuoni uendelevu wake kama bado upo ama utaweza kuendelea kuweko kwa miaka 10, 20 au 30 ijayo. Kwa sababu nyingi ambazo zinajitokeza, kwanza, mapito ya Wanyama, maarufu kama shoroba, nyingi zimevamiwa na wananchi. Zinavamiwa kwa sababu hatukuwa na mipango bora ya ardhi kwenye maeneo yetu. Pia kuna ongezeko la idadi ya watu na kuna ongezeko la matumizi ya ardhi. Siku zote napenda kusema ardhi haiongezeki, idadi ya watu inaongezeka, mahitaji na utumiaji wa ardhi unaongezeka kwa kasi kubwa kwa sababu ya idadi ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, ni lazima Serikali mwone namna gani ardhi yetu tunapangia matumizi bora na kuiwekea sheria; kama ambavyo tumetungia sheria maeneo yetu ya hifadhi, hivyo hivyo ukienda kwenye maeneo ya kilimo haina budi kuwa na sheria maalum ili wasiingiliane. Hivyo hivyo kwa wafugaji itatusaidia angalau kupunguza migogoro ambayo inajitokeza kwa wingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili, Hifadhi ya Ngorongoro. Kwanza tunamshukuru sana Mheshimiwa Mama Samia, katika speech zake zilizopita ameweza kuonyesha kwamba tunahitaji kuendelea kuilinda Hifadhi ya Ngorongoro kwa nguvu zetu zote. Hifadhi ya Ngorongoro ni Kivutio cha Asili, na ni Hifadhi ya Urithi wa dunia toka mwaka 1979 na ni hifadhi ambayo inatambulika kama Hifadhi Mseto. Ni hifadhi ambayo ina wanyamapori na shughuli za binadamu na makazi ya binadamu humo ndani. Kwa hiyo, siioni Ngorongoro ya miaka 20 ijayo kwa sababu, matumizi mseto ilikuwa ina-apply miaka ya nyuma, lakini siyo leo. Leo shughuli za kibinadamu zikiongezeka, ule uhifadhi tunaotamani kuuona Ngorongoro utapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza sana Mhifadhi Mkuu wa Ngorongoro, wameanza kuonyesha mfano, kwa sababu Ngorongoro sasa hivi wamehama; Makao Makuu ya Hifadhi ya Ngorongoro imehama kutoka kule Ngorongoro iliko hifadhini na kuhamia Karatu. Ni nia ambayo ilikuwepo muda mrefu, haijawahi kutelezwa, lakini leo imetekelezwa. Nampongeza sana Mhifadhi wa Ngorongoro na timu yake nzima, na bodi yake kwa hatua hii muhimu ambayo sasa itatoa mwelekeo mzuri wa kuendelea kuifanya Serikali ipunguze matumizi ya watu na binadamu ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro ili kuendelea kuilinda Ngorongoro ile ambayo tunaifahamu ilikuwa zamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma ripoti ya CAG, ameonyesha mambo mengi kuhusiana na Hifadhi ya Ngorongoro. Kuna tatizo la magugu vamizi, ambayo yanahatarisha Wanyama. CAG kwenye ripoti yake ameieleza vizuri sana. Amesema kwamba management wamejitahidi kuondokana na hiyo, lakini bado kuna mkwamo. Kwa hiyo, Wizara muone namna gani ya kukabiliana na hayo magugu vamizi ili tuendelee kuona Ngorongoro inastawi na inaendelea kuwa urithi wa dunia kama ambavyo imetangazwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya tatu, kuna mgogoro wa muda mrefu kati ya wananchi wa Kata ya Buger na Hifadhi ya Msitu Mara ambao unalindwa na TANAPA. Niseme yafuatayo: mwaka 2013 mwananchi mmoja alipigwa risasi mguuni na Askari wa TANAPA; tarehe 25 Mei, 2015 mwananchi mmoja alipigwa risasi akafariki; tarehe 28 Oktobam 2020 siku ya kupiga kura wananchi wa TANAPA waliwapiga risasi ng’ombe kumi wa mama mmoja mjane kwenye ile kata. TANAPA waliahidi watamfidia yule mama, lakini mpaka leo yule mama hajapata fidia hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 28 Desemba, 2020, watu saba waliingia kwenye msitu ule wa hifadhi, walikuwa wanakwenda kuchimba madini. Sitetei watu wanaoingia na kuvamia hifadhi na kutaka kuharibu hifadhi zetu, nachukizwa na utaratibu unaofuatwa baada ya hapo. Kama hao watu ni wahalifu, sheria zipo, tumezitunga ndani ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hao watu saba waliongia kwenye huo msitu, watu wanne mpaka leo hawajulikani walipo. Watu watatu walifanikiwa kutoroka, watu wanne inasemekana walichomwa mpaka kufa na Askari wa TANAPA. Haya ni mambo ambayo hayakubaliki. Sitetei uhalifu, lakini kuna sheria za kumchukulia hatua mhalifu yeyote. Sheria ziko very clear. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeshakuwa ni utamaduni wa kudumu wa mgogoro kati ya wananchi hawa wa Buger na Askari wa TANAPA. Ni eneo pekee ambalo Askari wa TANAPA hajawahi kukwaruzwa na mwananchi yeyote, ukilinganisha na maeneo mengine, labda inawezekana askari akauawa na wananchi kwa hasira; lakini kwa jinsi ambavyo wale wananchi walivyo, hakuna Askari aliyekwaruzwa wala kutolewa unyayo au kufanywa chochote kile, hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri, tuone namna bora ya kumaliza mgogoro huu. Leo ninapoongea hapa askari wale wako kule, nasikia wanarekebisha beacon, ambao ni mgogoro wa muda mrefu. Hatujapata suluhisho, lakini tunakwenda tena kuendelea ku- create matatizo ambayo yanaendelea kujitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, tuone namna bora ya kumaliza tatizo hili ili wananchi wale wakae kwa amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama amabvyo msemo maarufu unavyosemwa, kwamba maji ni uhai kweli maji ni uhai, na kwa ajili ya ustawi wowote wa jamii ni lazima kuwepo na uhakika wa upatikanaji maji safi na salama. Suala la upatikanaji wa maji safi na salama mdau wa kwanza kuhakikisha wananchi wanapata maji ni Serikali, ihakikishe wananchi wanapata maji katika maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama haitoshi kwenye baadhi ya maeneo, kama endapo Serikali kama inachelewa kupeleka huduma hii wananchi wanaamua wenyewe kujianzishia miradi yao kwa mujibu wa taratibu ili mradi wapate maji kwa ajili ya wa ustawi wa jamii yao. Miaka ya 1990 katika Wilaya ya Karatu kulikuwa kuna shida kubwa sana ya upoatikanaji wa maji. Ulipofika mwaka 1999 wananchi wa Karatu waliamua wenyewe, pamoja na viongozi wao wa wakati huo kujitafutia ufumbuzi kuhakikisha wanapata maji katika maeneo yao. Katika vijiji sita katika Mji Mdogo wa Wilaya ya Karatu, waliamua kuchangisha wenyewe fedha zao, kuchimba maji na kutafuta maji. Walihakikisha kwamba wanataka kupata uhakika wa maji. Ilipofika mwaka 2002 wananchi wa Karatu wakaanzisha mradi wa maji maarufu kwa jina la KAVIWASU. Ni mradi ambao ulikuwa umebeba na unatoa huduma katika vijiji sita ndani ya Mji wa Karatu. Wananchi hawa walihakikisha kwamba wanaendeleza mradi huu kwa fedha zao na kwa gharama zao wenyewe, na walisajili mardi huu kama bodi ya wadhamini chini ya vijiji hivyo sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, ilipofika mwaka 2022 mradi huu ulitimiza miaka 20 kwa huku wananchi wakiendelea kujiendesha wenyewe kwa kuhakikisha wanasambaza maji, wanapata maji na mradi unaendelea kukua. Lakini mradi huu mara ya kwanza ulikuwa unatumia maji mtiririko, kwa maana ya maji ya msimu wa mvua, lakini baadaye wananchi wakajiongeza wakaanza kuchimba na visima virefu ili kuhakikisha upatikanaji wa maji wa uhakika kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu katika miaka 20 uliodumu kabla ya mwaka jana maamuzi yaliyofanyika ambayo nitayaeleza uliweza kuhakikisha ndani ya vjiji hivyo sita katika Mji wa Karatu asilimia 76.8 ya wananchi wanapata maji. Lakini kama haitoshi mtandao wa maji uliweza kufikia kilomita 478.4, na wananchi ambao wamejivutia maji majumbani walifika takriban kaya elfu tatu na zaidi. Vilevile mradi huu ulikuwa unazalisha lita milioni nne kwa saa, katika mji wa Karatu. walikuwa na ma-tank ya kuhifadhia maji 23, ma-tank ambayo yanakidhi lita tofauti tofauti kuanzia elfu thelathini na tano, elfu kumi na tano, elfu saba na kuendelea. Lakini walikuwa na visima virefu nane vya uhakika vya kuhakikisha maji yanapatikana mwaka mzima na wananchi katika vijiji hivi wanapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia walikuwa wana Public DP, yaani machoteo ya maji ya wananchi wa kawaida 128, na yote yalikuwa ni active na yanapatikana bila shida. Sasa shida ikaja mwaka jana, Mheshimiwa Waziri amekwenda Karatu amevunja mradi huu. Wananchi wa karatu wanauliza; kwa mafanikio haya ambayo wao wenyewe kwa fedha zao mradi huu umechangiwa na wananchi asilimia 100 hakuna hata shilingi 10 ya Serikali iliyokwenda pale; ni sababu zipi zilifanya Wizara Kwenda kuvunja mradi huu? Wananchi hawa walikuwa na tatizo la maji miaka yote hawakupata hata shilingi 10 kutoka Serikalini, wakaamua wenyewe kwa jitihada zao wakajiletea mradi wa maji, wakausajili kwa utaratibu unavyotakiwa, kwa nini Wizara mmeend akuvunja mradi huo wa wananchi?

Mheshimiwa Naibu spika, lakini kama haitoshi kuwepo miradi kama hii Karatu si ya kwanza, kuna miradi mingine ambayo imefanya vizuri sana katika Jimbo la Hai. Nilikuwa naongea na Mheshimiwa Mbunge pale asubuhi kuna mradi wa Uroki, Bomang’ombe, kuna mradi wa Losaa-Kia kuna mradi wa Machame kuna mradi wa Lyamungo. Miradi hii inafanana kabisa na mradi ule ule ulioko Karatu, na miradi hii na inafanya vizuri sana. Mheshimiwa Mbunge amenipa taarifa pale asubuhi miradi hii bado ipo kwa upande wa Hai.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunataka kujua Karatu wamewafanya nini mkaenda kuvunja huu mradi? Na kama kulikuwa kuna shida kwa nini hamkukaa na wananchi, mkawafuata na mkapata maoni mkataka kujua? Mheshimiwa Waziri mmeenda na hoja nyepesi sana, mmesema mradi wa KAVIWASU ulikuwa unatoza maji ghali, mkaanziha mradi wa Serikali unaitwa KARUWASA mwaka 2014. Wakati mnaanzisha mradi wa KARUWASA, KAVIWASU ilikuwa inashida gani? Sisi wananchi tunajua kulikuwa hakuna shida, nyinyi mkaanzisha mradi mwingine wa Serikali ndani ya eneo lile lile ambalo wananchi walijipatia maji wenyewe. Huu mradi wa KARUWASA mliouanzisha Serikali ulikuwa unatoa huduma kwa asilimia 30 tu. Ilikuwa ina mtandao wa maji kilomita 58, ilikuwa inazalisha maji lita 1,000,000…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu, na mimi nitakuwa na hoja moja tu kuhusiana na maduka ya kubadilishia fedha za kigeni hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, tunakumbuka mwaka 2018 Serikali iliunda task force na ikafanya uvamizi katika maduka haya ya kubadilishia fedha na hususan katika Kanda ya Kaskazini, mikoa ya Arusha na Kilimanjaro ndio ambao wameathirika kwa kiwango kikubwa. Task force hizi zilivamia maduka haya zikachukua fedha, zikachukua vifaa mbalimbali ikiwemo computers, EFD machines, baadhi ya wafanyabiashara wakachukuliwa hati za ardhi, na kadhalika. Na leo nazungumza hii ni kama mara ya tatu au sio ya nne ndani ya Bunge hili kutaka kujua kauli ya Serikali kuhusiana na wafanyabiashara hawa ambao wameporwa fedha zao toka mwaka 2018 mpaka leo hakuna muafaka wowote uliofikiwa kuhusiana na jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mmechukua mpaka hati za ardhi za watu, mmechukua fedha cash, mmechukua vifaa mbalimbali, wafanyabiashara hawa hawajui hatima yao. Ni lini Serikali mtafikia muafaka kuhusiana na mashauri haya ya wafanyabiashara hawa ambao mlikwapua fedha zao katika maduka ya kubadilishia fedha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kama haitoshi mmeunda tena task force mpya, mmeenda kwa wafanyabiashara hawa kuwaambia tena wanadaiwa. Sasa mmewachukulia kila kitu, mmewanyang’anya, bado mmeunda task force tena kuwaambia wafanyabiashara hao wanadaiwa, kwa nini? Na kwa nini mnafanya kazi kwa task force tu ya kutishia watu na si kuleta amani na muafaka ili watu wafanye biashara kwa uaminifu? (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, naomba tupate majibu ya kina na ya ukweli. Na wafanyabiashara hawa wanataka kujua hatima ya fedha zao mlizozichukua bila utaratibu.

Mheshimiwa Spika, na niliwahi kusema hapa, hawa watu wanavyofanya biashara wana leseni za biashara, wamefuata taratibu zote, hakuna mtu ambaye alikuja tu akawa anafanya biashara hajafuata taratibu. Mliwatambua, walifanya biashara kwa utaratibu, kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni. Bado mkaja mkawanyanyasa na kuwavamia na kuwachukulia fedha na kila kitu. Naomba kupata majibu Mheshimiwa Waziri kwa sababu ni mara nyingi nimeshaongelea suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kama haitoshi mmeweka masharti mapya magumu ya watu wanaotaka kufanya biashara ya kubadilisha fedha kwa kuanzisha maduka. Mmeweka masharti magumu sana ambayo kwa kweli, hayawezi kutekelezeka. Mnataka mtu ili apewe leseni hii awe na fedha shilingi bilioni moja ndio aweze kufungua, na tena katika hiyo bilioni moja ili aweze kupata sasa leseni na kibali, maana yake awe na fedha asilimia 70 ya hizo fedha, maana yake ni shilingi milioni 700. Hivi kwa nini kuna ugumu kwenye jambo hili katika kufanya biashara hii?

Mheshimiwa Spika, huko nyuma watu walifanya biashara, Arusha ndio biashara ambayo ipo na Kilimanjaro kwa sababu ni miji ya kitalii. Sasa kwa nini mnaweka masharti haya magumu kiasi hicho? Kuna nini kimejificha hapa Mheshimiwa Waziri?

Mheshimiwa Spika, lakini kama haitoshi wako baadhi ya wafanyabisahara pamoja namasharti hayo magumu, wako baadhi ya wafanyabiashara ambao wamekidhi hivyo vigezo. Wameleta maombi, lakini mpaka leo wana karibu miaka miwili, mitatu, hamjatoa leseni, kuna nini hapa? Kuna nini ambacho kimejificha? (Makofi)

Mheshimiwa Waziri, ningetamani nipate majibu ya masuala haya niliyoyaeleza, lakini kama haitoshi tunataka kujua hii biashara ya kufungua maduka ya kubadilishia fedha ndani ya nchi hii, kama mtangaze ni janga mseme ni janga, kama mnaona ni biashara ambayo ni hatari muwaambie. Hawa wafanyabiashara wamekaa hawajui hatima yao, hata hao wapya ambao wamekidhi vigezo wameleta kwenu bado mmekaa kimya, kuna nini hapa ambacho kinaitishia Serikali na mnapata kigugumizi kuhusiana na suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru. Langu ni hilo na kama sitaridhika nafikiri tutakutana kwenye shilingi baadae Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo, wa Mwaka 2016
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Miswada iliyoko mbele yetu, mchango wangu utajikita katika Muswada wa kuanzisha Taasisi ya Utafiti wa Kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni takriban asilimia 73 ya Watanzania hutegemea kilimo na ni muhimu sana ili kilimo hiki kimnufaishe Mtanzania au Watanzania hawa wa asilimia 73 ni lazima hiki kilimo kiwe na manufaa, kiwe na tija lakini ni lazima kiwe ni kilimo ambacho tafiti zitafanywa zitaweza kuwasaidia kuboresha kilimo chao ili kiweze kuwasaidia kwa maana ya uchumi, mahitaji ya familia na mahitaji ya nchi kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tumekuwa tukianzisha hizi taasisi. Hii ni moja tu ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo lakini tunakuwa na taasisi nyingi na Muswada huu unapendekeza kuanzisha taasisi hii ambayo itakuwa ina Bodi, Menejimenti na Itakuwa na Baraza la Taifa la Utafiti. Kikwazo kikubwa ambacho mara nyingi tunakiona ni uwezeshwaji wa hizi Taasisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa kuna changamoto kubwa sana, Taasisi zinaundwa, zinaachwa, fedha inapewa „kiduchu‟, inapewa OC, zile za other charges lakini fedha kwa ajili ya maendeleo na fedha kwa ajili ya shughuli maalum hasa ya utafiti inakuwa ni mtihani na mara nyingi hili tumeliona. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Wizara na Serikali kwa ujumla kwamba ni muhimu sana mtakapokamilisha mchakato huu kuhakikisha hii taasisi inapatiwa fedha ya kutosha kuhakikisha inaendesha shughuli zake, inafanya utafiti ili iweze kuwasaidia wakulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na fedha, wanahitaji pia kupata fedha au wanahitaji kupata fedha za uwezeshwaji wa kununua hivyo vitu ambavyo watafanyia utafiti au ambavyo vitaendana na teknolojia ya kisasa zaidi ili kuwasaidia na kurahisisha ufanyaji wao wa kazi. Kwa hiyo, ni muhimu sana, pamoja na kwamba tunapitisha hii Miswada, tunaunda hizi Taasisi ambazo ziko nyingi lakini bila kuwezeshwa kwa bajeti ya uhakika ya maendeleo mwisho wa siku hizi taasisi zitabaki tu kwenye makaratasi itakuwa hakuna kazi nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi hii itakuwa ina kazi ya kuratibu utafiti, ufuatiliaji na tathmini, kwa hiyo, ni muhimu sana inapofanya tathmini yake, inapofanya tafiti yake, haya matokeo yanayopatikana ni lazima yawe-shared yaweze kushirikisha na mrejesho uweze kuwafikia wadau husika kwa maana ya wakulima au wale wote ambao wananufaika kwa namna moja ama nyingine. Kwa hiyo, haya ni masuala ya msingi sana kuyazingatia kuona tathmini hii inayofanyika ni lazima wadau washirikishwe, ni lazima wadau waweze kunufaika nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii taasisi sasa ni lazima iangalie namna ambavyo itaungana au itaunganisha nguvu za pamoja na vyuo vyetu vikuu ambavyo vimekuwa vikifanya tafiti mbalimbali. Kwa hiyo, tusiwaache pembeni pia wataalam wetu, kwamba leo tunaanzisha hii Taasisi lazima pia tuangalie namna gani tutaendelea kushirikisha na kuunganisha nguvu za pamoja na hivi vyuo vikuu ambavyo vimekuwa vikifanya tafiti miaka yote kabla ya kuanzisha chombo hiki. Kwa hiyo, haya ni mambo ya msingi ya kuzingatia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya kuanzisha Taasisi hii, tunatarajia kwamba ni lazima Serikali sasa itumie takwimu hizi, itumie matokeo ya tafiti hizi katika upangaji wa mipango yake, katika upangaji wa bajeti, katika kukifanya kilimo kiwe na tija kwa wakulima. Kwa hiyo, ni lazima hili likazingatiwa kuona tunaanzisha taasisi inakuwa na matokeo fulani, inakuwa na mitazamo fulani, inakuwa ina ushauri fulani kuhusiana na masuala haya ya kilimo, ni vyema Serikali ikayafuata, ikayachukua, ikawa ni dira yake ya kupangia bajeti na mipango mbalimbali ya sekta ya kilimo hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie sasa kwa kuchambua kidogo Muswada na kutoa mapendekezo. Ukisoma Muswada huu wa Kiswahili, kwenye heading pale inahitaji kufanyiwa marekebishao kwa sababu kule juu inasomeka Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi, lakini content zote ni Taasisi ya Kilimo na mwanzo kabisa wa heading hapa kwenye Kiswahili, ya Kiingereza iko sawa, lakini kwenye Kiswahili imeanza, ukurasa wa kwanza iko sawa, kwamba ni Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo, lakini ukiendelea page ya pili mpaka ya mwisho inasomeka Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi na siyo Mifugo. Kwa hiyo, nadhani inahitaji kufanyiwa marekebisho ili iweze kuleta maana sahihi kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kifungu cha 5(2)(a) kinasema, Mwenyekiti wa Bodi atateuliwa na Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha 8(1) pia kinaeleza, Mkurugenzi atateuliwa na Rais. Kama ambavyo Kambi ya Upinzani imependekeza ni lazima tuondoke kwenye huu mfumo wa uteuzi, tuingie kwenye mfumo wa ushindani, tushindanishe watu wenye sifa, tutangaze hizi kazi, ni kazi ambazo kwa kweli zinahitaji utaalam na watu ambao wako tayari. Kwa hiyo, ni lazima tuondokane na huu mfumo wa uteuzi ambao umekuwa ni mwingi mno wa kubebana. Ni lazima tutoke huku tushindanishe hizi kazi, watu wenye sifa waombe, wachujwe kwa vigezo ili mwisho wa siku waweze kupata hizi nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukienda Kifungu cha 8(2)(d) wanasema katika uteuzi wa huyu Mkurugenzi anasema awe mbunifu, najiuliza hivi utapimaje ubunifu wake wakati ndiyo uko kwenye uteuzi? Sina hakika kama unaweza ukapimika ubunifu wa mtu kabla hujampa task fulani aifanye. Kwa hiyo, nadhani hapa inahitaji kurekebishwa labda ibaki tu yale maneno mengine kwamba awe na uzoefu na uadilifu, lakini ubunifu sina uhakika kutakuwa na kigezo gani cha kumpima ubunifu wake. Kwa hiyo, nadhani inahitaji kufanyiwa marekebisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kifungu cha 21(1)(c) kinazungumzia kuanzisha Kamati ya Kitaifa za kuratibu tafiti za mazao. Mwanzoni kwenye vifungu vingine inaeleza mfumo wa taasisi, kutakuwa kuna Bodi, kutakuwa kuna Menejimenti, kutakuwa kuna Baraza la Ushauri la Utafiti la Kitaifa, lakini huku tena mnasema kutakuwa kuna Kamati za Kitaifa za kuratibu utafiti wa mazao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tunaweza tukawa na Kamati na Mabaraza mengi ambayo mwisho wa siku ukiyapima au pamoja kuyapima yatakuwa na gharama kubwa za uendeshaji lakini ukipima hata matokeo yake yanaweza mengine yanaingiliana kazi zake au majukumu yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani ama Mheshimiwa Waziri atupe ufafanuzi wakati anahitimisha ama hili liweze kufanyiwa marekebisho na kuona namna gani linaondolewa ili kupunguza hizi Kamati na haya Mabaraza ambayo yamekuwa mengi, mwisho wa siku inagharimu fedha nyingi ikiwa na matokeo machache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimalizie tu kwa kusema kwamba ni lazima Serikali iangalie umuhimu wa kuwezesha hizi taasisi ambazo zimekuwa zikianzishwa, siyo tu kuwapa fedha za mishahara, fedha nyingine za OC, lakini fedha za maendeleo hamuwapi. Kwa hiyo, ni lazima Serikali muwajibike kuwapa fedha ili hiki kinachokusudiwa katika Muswada huu na kuwalenga Watanzania asilimia 73 ambao wao wanategemea kilimo, basi kiweze kuwa na tija na manufaa, kwao binafsi, jamii zao na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Shirika la Mawasiliano Tanzania wa Mwaka 2017
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Muswada huu ambao umewasilishwa mbele yetu siku ya leo, na naunga mkono maoni ya Kambi ya Upinzani ambayo yamewasilishwa hapa. Ni vizuri sana Serikali mkatupa majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuongezea mchango wangu, napenda kwanza watuambie ni kwa nini leo wanatuletea mapendekezo haya ya kutoka kuwa Kampuni ya Simu na kwenda kuwa Shirika la Mawasiliano. Mheshimiwa Waziri hapa ameeleza kwamba Muswada huu sasa unaitoa TTCL kutoka kampuni kwenda shirika kwa mambo ambayo ameeleza hapo; moja likiwa ni kulinda usalama wa nchi. Tunajiuliza, ilipokuwa kampuni ilikuwa haiwezi kulinda usalama wa nchi? Jambo la pili, amesema kukuza uchumi; ilipokuwa Kampuni ya TTCL ilikuwa haikuzi uchumi, leo tunapobadilisha kwenda shirika ndiyo itakuza uchumi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kutoa huduma za mawasiliano kwa jamii; ilipokuwa kampuni ilikuwa haitoi huduma, leo tunapofikiria kuwa na Muswada wa kwenda kuwa shirika, je, ndiyo itaweza kutoa huduma hizo za mawasiliano kwa jamii? Nadhani kinachokosekana sio ubadilishaji wa sheria kutoka kampuni kwenda shirika, kinachokosekana ni Serikali kutokuziwezesha hizi kampuni ambazo zimeanzishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, TTCL imekufa kwa sababu ilikuwa haiwezeshwi na Serikali, haipewi ruzuku kwa wakati, haiboreshwi, haiendani na ushindani uliopo. Kwa hiyo,leo wakituletea tu kusema wanabadilisha, kama hawatahakikisha hilo shirika ambalo leo tunataka kulipitisha hapa litapatiwa ruzuku ya kutosha, maana yake litaendea kuwa kama ambavyo leo liko katika hali mbaya sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo hotuba yetu ya Kambi imesema, tunahitaji pia kuhakikisha namna gani Serikali inatoa ruzuku kwa wakati na kuwepo na vyanzo vya uhakika vya kuwezesha hili Shirika la Mawasiliano la Taifa. Kwa hiyo,ni muhimu sana, pamoja na kuwa na sheria nyingi au sheria tu kwenye vitabu, lakini bila uwezeshaji bila shaka hakuna kitu kitakachofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tunapofikiria wananchi wetu waweze kupata mawasiliano kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema, ni mawasiliano ya namna gani, yanaweza kuwa affordable na wananchi wa level ipi na kwa kiwango gani. Kwa hiyo, pamoja na kwamba tunaona tunaanzisha shirika, lakini lazima kuwepo na urahisi wa upatikanaji wa mawasiliano kwa wananchi kule vijijini kuhakikisha mawasiliano yanapatikana kwa wakati na yanaweza kuwa affordable kwa kila mwananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nitoe mapendekezo katika Muswada kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha saba (7) kimeelezea Board of Directors; napendekeza pale kwenye uwakilishi wa members wa Board of Directors wameleta mapendekezo kwamba upande wa Zanzibar awepo mwakilishi mmoja kati ya five members watakaokuwa kwenye bodi. Kama kweli tunaitambua Zanzibar kama sehemu ya nchi hii, kuwapa nafasi moja sio kuwatendea haki, nafikiri kuwatendea haki ni kuwaongezea nafasi, mbili zitoke Zanzibar na nafasi tatu zitoke Tanzania Bara. Kwa hiyo, napendekeza pale katika kifungu cha saba (7) waweze kuongeza idadi ya wajumbe kutoka Zanzibar kwenye hiyo Board of Directors; wawe wawili badala ya mmoja kama ambavyo wameweza kuandika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo, katika ibara hiyohiyo ya 7(7), wamesema pale napenda kuongeza maneno kwamba The Minister in consultation with the Board anaweza ku-publish mambo yote ambayo yanaweza kufanyiwa marekebisho. Tusimwachie tu Waziri mwenyewe abebe hili jukumu, lakini Waziri afanye mawasiliano na bodi yake. Sasa kutakuwa hakuna maana ya kuwa na bodi kama Waziri anaweza tu akawa anaamua kila kitu. Kwa hiyo,ni vizuri Waziri anapofanya mambo yoyote yale, ni lazima afanye consultaion na bodi yake aliyounda ili kuwepo na ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika ibara ya tisa (9), wanapendekeza kwamba Waziri anaweza kuzi-direct bodies; ni sawa, anaweza kutoa maelekezo, lakini sheria inasema maelekezo yote yatakayotolewa na Waziri ni lazima bodi ifuate na itimize. Nadhani tusiweke kipengele hiki cha kuilazimisha bodi; Waziri ni mtu, ni binadamu, leo anaweza akatoa maelekezo akiwa kwenye hali ya hasira au ana frustration au anatoa maelekezo ambayo mwisho wa siku hayawezi kuleta ufanisi wa shirika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri tuache kipengele kiseme kwamba kama Waziri atatoa mapendekezo kwa bodi, basi iwe ni bodi kuamua kuyafuata, kusiwepo na ulazima wa kisheria au uhitaji wa kisheria kwamba lazima yale ambayo yatatolewa na Waziri yaweze kufuatwa. Kwa hiyo, napendekeza kwamba kifungu cha tisa (9) kuondoa maneno ya mwisho pale baada ya neno act kwamba and the Board shall give effect to any direction given to it. Kwa hiyo, ibaki tu maneno ambayo yatasomeka hapo haya mengine yaondoke.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema haya kwa sababu nimepeleka schedule of amendment, naambiwa nimechelewa muda hautoshi wakati kuna mambo mengine ambayo tunaweza kuyapendekeza kwa ajili ya Muswada huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa pia mapendekezo katika kifungu cha 15; uzoefu katika appointments hizi za Director wa shirika, kama ilivyosema hotuba ya Kambi ya Upinzani, unaposema miaka nane ni mingi sana,
napendekeza iwe experience ya miaka mitano. Tunaangalia experience, ndiyo ni jambo moja, lakini kuna uadilifu, kuna mambo mengine mengi sana ya kuweza kuona mtu gani anafaa katika nafasi fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweza kusema awe na experience ya miaka nane wakati mtu mwenyewe ni mbovu, hana uadilifu wowote ana upungufu mwingi. Kwa hiyo, tusiweke kwamba ni lazima awe na experience ya miaka nane, napendekeza kuwe na experience ya miaka mitano kwa huyo ambaye atateuliwa kuwa Director wa shirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie mchango wangu kwa kuendelea kuisisitizia Serikali kwamba, hatuwezi tu kusema tunabadilisha sheria kila kukicha, leo tunabadilisha sheria hii kutoka Kampuni ya TTCL kwenda Shirika la TTCL halafu bado tunakuja na sheria nyingine nyingi ikiwemo hizo ambazo tumeshapitisha kwenye Bunge hili ya kuzuia mawasiliano, kudhibiti mawasiliano ya watu, kuzuia watu kutoa maoni yao na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Serikali ni vizuri ikawa consistency na mambo inayoyafanya katika utungaji wa sheria. Kama tunatunga sheria hiyo tukilenga kumaanisha wananchi wote waweze kupata mawasiliano kwa kadri inavyowezekana, basi tusije na sheria nyingine ambazo zinaweza kuwa zinanyima uhuru wa watu kupata mawasiliano au kutumia mawasiliano kwa kadri ambavyo yataweza kupatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Fedha wa Mwaka 2022
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu ya marekebisho ya sheria. Nitachangia katika maeneo mawili na baadaye nitatoa ushauri.

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kuhusiana na Sheria ya Ushuru wa Mafuta ya Barabara Sura Namba 220. Serikali inapendekeza hapa kutoa msamaha wa kodi katika miradi mahiri na mahiri maalum. Sasa kupitia uzoefu huko nyuma, kama ambavyo ameeleza pia Mheshimiwa aliyetoka kuongea, mara nyingi hii misamaha inaweza ikatumika vibaya kwasababu wanaofanya haya mambo sio Malaika na watu. Kwa hiyo inaweza ikawa ni kichaka cha watu kupitisha bidhaa kupata kwa unafuu na kukwepa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo amesema Mheshimiwa aliyetoka kuongea huko nyuma tulitoa misamaha kwenye miradi ya migodi watu wakawa wanapitisha mafuta yanaingia kwa mujibu wa utaratibu na ikifika migodini mafuta yanatoka yanakwenda mtaani na hivyo watu wanakwepa kodi. Kwa hiyo pamoja na mambo ambayo mmeeleza kuhimarisha mfumo wa usimamizi, kufanya ufuatiliaji na kuweka kipindi maalum ambacho kitaainishwa katika kanuni sasa haya yanayosemwa ni vema yakasimamiwa ipasavyo ili kuhakikisha malengo haya yaweze kufikiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini kama haitoshi ni lazima pia kupitia taarifa za utekelezaji ambazo zinakuja Bungeni, tuambiwe hii miradi mahiri na mahiri maalum ni ipi? Kwasababu ukiiacha tu hivyo wananchi wa kawaida wanaweza wasielewe, na hata sisi Wabunge wakati mwingine tunaweza tusiielewe; kwamba hii miradi mahiri na mahiri maalum ni ipi. Ni lazima iainishwe na tujue kwamba miradi hiyo ni ipi na itapewa misamaha na kwamba lazima kuwepo na ufuatiliaji na udhibiti ili kuhakikisha kwamba kweli mafuta hayo hayatotumika vibaya, msamaha huu uliotolewa hautatumika vibaya.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nichangie pia katika Sheria ya Ushuru wa Bidhaa Namba 147. Serikali inaleta mapendekezo hapa ya suala la mvinyo au wine, kwamba bidhaa zinazotoka nje wanaongeza ushuru kutoka shilingi 2,466 kwa lita hadi shilingi 5,600 kwa lita.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwa takwimu ni figure kubwa ambazo zinaongezeka; lakini sababu ya hayo marekebisho mnatuambia ni kulinda viwanda vya ndani. Sasa, kulinda viwanda vya ndani kwa bidhaa zinazotoka nje hiyo inaweza ikawa ni sababu mojawapo katika sababu nyingine nyingi. Inawezekana nyinyi mmelenga kwa mtizamo wakupata mapato halafu mkajificha kwenye kichaka cha kusema tunalinda viwanda vya ndani.

Mheshimiwa Spika, bidhaa zinazotoka nje kwenye huu mvinyo au wine soko la ndani bidhaa inayotoka nje ipo kwa kiwango cha asilimia 70. Nieleze hivi, bidhaa za nje, wine inayotoka nje ya nchi kwenye soko letu ipo kwa asilimia 70 wine inayozalishwa nchini kwa bidhaa za ndani ipo kwa asilimia 30. Sasa mnasema matalinda viwanda vya ndani, sawa mtalinda viwanda vya ndani, lakini kwa nini viwanda vya ndani vinaingia soko kwa asilimia 30? Hii inamaanisha kwamba kuna changamoto.

Mheshimiwa Spika, moja ni ubora wa wine husika. Tunapolenga kuhakikisha kwamba tunaongeza ushuru huo ili kulinda bidhaa za ndani lazima tuangalie wazalishaji wetu wakoje? Mazingira yao ya uzalishaji yakoje? Bidhaa inayozalishwa hapo inau bora? Leo hutomlazimisha mtu anunue wine kutoka ndani ilhali haina ubora akinywa labda inakereketa hapa kwenye koo au akiinunua unakuta haina ule ubora unaotakiwa. Kama lengo ni kumsaidia huyu mkulima wa mvinyo hapa nchini ni lazima kuhakikisha kuwa anatengenezewa mazingira na kumwezesha atoe bidhaa ambayo ina-quality inayoingia sokoni akihakikisha kwamba anaingia kwenye soko na anashindana.

Mheshimiwa Spika, lakini kama haitoshi lazima wajitangaze na kuhakikisha namna gani tunawasaidia kupata mitaji kama Serikali, na inawezekana hawana mitaji ya kufanya hii biashara, kwa hiyo lazima tuangalie pia kwenye suala la kuwawezesha kimitaji wafanikiwe ili nao waweze kuingia sokoni ili sasa ile asilimia 70 iwe ya ndani na asilimia 30 iwe ya nje; kwa hiyo lazima tutazame kwa mtazamo huo. Tunaposema kulinda viwanda vya ndani tuiseme kwa matendo kwa kuwasaidia. Ni vyema sana Serikali ikalitazama hili.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kuhusu ushauri wa jumla. Maoni ya Kamati yameeleza vizuri sana, wamependekeza kuimarisha kitengo cha utafiti wa sera za mapato, ni jambo muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, kitengo hiki ni lazima kiimarishwe ama ki-rasilimali watu au kifedha au kiujuzi. Kwanini nasema hivi, ni kwa sababu hawa ndio ambao hatimaye kupitia Wizara yako Mheshimiwa Waziri wanatuletea mapendekezo hapa Bungeni ya aina ya vyanzo vya mapato vinavyokuja hapa Bungeni tuvipitishe ili Serikali muweze kuenda kutekeleza.

Mheshimiwa Spika, huko nyuma tumeona mapendekezo ambayo yamekuja, na yako mengine ambayo leo ni kelele kwa wananchi. Kwa mfano huko nyuma kuna sintofahamu kubwa sana kwenye kodi ya majengo ambayo ilipendekezwa, kwenye tozo ya miamala ya simu na kibenki ambayo juzi umetoa kauli hapa ya kusema unaziondoa. Haya yote yanakuja na leo tunakuja kufanya marekebisho maana yake kuna tatizo mahali. Inawezekana katika kufikiria vyanzo vipi vya mapato hiki kitengo kuna shida ama ya uwezeshwaji ama upungufu wa rasilimaliwatu ama mafunzo na ujuzi.

Mheshimiwa Spika, tukitaka tuone namna ya kufanikiwa katika aina ya mapato au kuwa na sera bora za mapato ambazo zitakuwa ni za uhakika na za uendelevu ni lazima tukiimarishe hiki kitengo, Kamati imeshauri vizuri sana. Kwa hiyo ni vema Serikali mkayatazama haya. Ni lazima tuwe na namna ya kumpunguzia mwananchi mzigo. Hizo tozo zimekuwa kelele. Ndiyo, mnafanya marekebisho lakini imekuwa kelele sana lazima tufikiri hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine muhimu, Waziri alisema juzi hapa, kwamba wanaenda kuhakikisha wanapunguza matumizi ya Serikali. Haya yaliyosemwa ni vema sana yakaonekana kimatendo. Wakati tunapitisha bajeti hapa, Waziri alipokuwa anahitimisha alisema hivyo hivyo, lakini leo pamoja na kusema hayo kwamba tunaenda kupunguza matumizi makubwa ya Serikali bado tunayaona. Mnasema mnayapunguza lakini leo ukiona mtaani Serikali mmenunua magari mapya, new model haya ambayo yapo sokoni sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali ikisema haya basi tuyaone kwa matendo. Tumetoka tu hapa kwenye bajeti tunakutana na magari mtaani. Lakini hata haya matumizi ya magari ya Serikali kwa kweli sijui tufanyeje kama Bunge, lazima yatizamwe kwa upya, magari ya Serikali baadhi, siyo yote, kwa kweli yanatumika ndiyo sivyo. Yako mengine yanapeleka maafisa na wakati huo huo wanatumia magari hayohayo kuwapeleka watoto wao shuleni, ndiyo yanayokwenda sokoni. Bosi akikaa ofisini ndiyo yanaenda kufanya kazi ya ziada. Inawapeleka watoto shule, inakwenda kuwachukua watoto shule, inakwenda sokoni. Yaani inaenda kufanya shughuli ambazo sizo. (Makofi)

Mheshimiwa spika, Waziri ulisema hapa kwenye bajeti yako, tunatamani kuona utekelezaji wa kivitendo si wa kimaneno. Haya ambayo mmeyasema tuyaone kweli.

Mheshimiwa Spika, na kuna siku ulipendekeza vizuri kweli, utakuta gari linamsubiri boss linakaa masaa sita au nane liko on. Sasa hayo pia ni miongoni mwa matumizi ambayo si sahihi ya fedha za walipa kodi. Tunataka kuona mwananchi anapunguziwa mzigo wa kodi zisizokuwa za lazima na tunataka kuona matumizi ya siyokuwa ya lazima yanapungua kwa Serikali. Kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema, sisi kama Wabunge tutaendeleza jukumu letu la kushauri na kupiga kelele. Tutapiga kelele kuhakikisha yale ambayo umeyanena tunayafuatilia na tuone utekelezaji wake kwa vitendo. Ahsante sana. (Makofi)