Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Dr. Elly Marko Macha (1 total)

MHE. DKT. ELLY M. MACHA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba Serikali yetu ya Tanzania ilisaini na kuridhia ule Mkataba wa Kimataifa wa 2006 kuhusu haki za watu wenye ulemavu, uliridhiwa, yaani ulikuwa ratified mwaka 2009. Utaratibu ni kwamba baada ya miaka miwili baada ya kuridhia, Serikali inatakiwa kuandika State Report na kuiwakilisha kwa ile Kamati ya Umoja wa Mataifa inayosimamia utekelezaji wa huo mkataba.
Mheshimiwa Spika, mpaka sasa Serikali yetu haijaandika hiyo State Report, sasa ni miaka minne overdue. Ni kwa sababu gani, Serikali yetu haijapeleka State Report kuhusu huo Mkataba wa Watu Wenye Ulemavu?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Macha, Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imeridhia mikataba mingi sana, kwa lengo la kuunganisha Taifa letu na matakwa yetu na Mataifa na Taasisi mbalimbali za Kimataifa ili kuweza kufungua milango ya huduma mbalimbali, mahitaji mbalimbali ya nchi na Mataifa ya nje ikiwemo na jambo ambalo Mheshimiwa Macha amelieleza.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali yetu imedhamiria kufungua milango na kutoa huduma na kuweza kuwafanya ndugu zetu wenye mahitaji maalum kuwa ni sehemu ya wachangiaji wakubwa wa shughuli mbalimbali za maendeleo nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tumefungua milango hiyo, Serikali ya Awamu ya Tatu, Serikali ya Awamu ya Nne imeweza kuwashirikisha kikamilifu Watanzania wote ambao wana mahitaji maalum na katika kuweza kuona katika kupata mchango wao ili pia waweze kutoa mchango wao kikamilifu, ikiwemo na mikataba hii. Mikataba hii baada ya kuwa tumeunda Serikali yetu, tutafanya mapitio ya kazi zote zile za Awamu ya Nne ambazo zilikuwa zimefikiwa na sasa tuweze kuunganisha na mkakati ambao Mheshimiwa Rais ameuweka wa kuunda Wizara inayoshughulikia eneo la hilo na baadaye itafanya mapitio na imeshaanza kufanya mambo mengi ya kuweza kuridhia mikataba yote au kupitia mikataba yote ambayo tunadhani inaweza kuwaunganisha Watanzania wote kuweza kuridhia jambo ambalo tumekubaliana nalo. Kwa hiyo, hili ni pamoja na lile ambalo Mheshimiwa Macha amelieleza.
Mheshimiwa Spika, kwa mkakati tulionao, Mheshimiwa Dkt. Possi ameanza kukutana na wadau wenyewe kuanza kupitia mikataba ile kuona kama ina tija kwa Taifa, ina tija kwa ndugu zetu Watanzania ili sasa tuweze kuridhia. Kwa hiyo, taratibu zinaendelea na pindi itakapokamilika, tutaweza kukushirikisha Mheshimiwa Mbunge.