Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Amina Saleh Athuman Mollel (17 total)

MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Watu wenye ulemavu wanapitia changamoto nyingi sana katika safari zao za kimaisha na mojawapo ni miundombinu isiyo rafiki kwa ajili ya kupata elimu:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua matatizo hayo ili kuwawezesha watu wenye ulemavu kufurahia matunda ya elimu kwa kuweka mazingira mazuri yatakayowasaidia kupata elimu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Molel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Wanafunzi Wenye Ulemavu wanahitaji mazingira bora ya kujifunzia na kufundishia pamoja na miundombinu rafiki katika maeneo yote ya kutolea elimu ikiwa ni pamoja na madarasa, jengo la utawala, maktaba, maabara na vyoo. Ili kuhakikisha kuwa miundombinu inaboreshwa kukidhi mahitaji ya wanafunzi wenye ulemavu, Wizara imechukuwa hatua zifuatazo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, imeandaa na kusambaza miongozo ya namna ya ujenzi wa majengo ya shule za msingi na sekodari pamoja na utengenezaji na ununuzi wa samani. Miongozo hiyo imeainisha mambo ya kuzingatia katika ujenzi wa majengo yote ya shule ili kupunguza vikwazo kwa wanafunzi wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika ujifunzaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua nyingine iliyochukuliwa na Wizara ni kuendelea kuhamasisha uanzishwaji wa shule na vitengo maalum vyenye mabweni kwa ajili ya kuandikisha wanafunzi wenye kiwango kikubwa cha ulemavu kwa lengo la kukabiliana na changamoto ya kutembea umbali mrefu na kuwapunguzia wazazi adha ya kuwapeleka na kuwarudisha nyumbani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutoa mafunzo ya elimu maalum kwa Walimu katika ngazi mbalimbali ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa Walimu katika eneo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kununua na kusambaza vifaa vya kielimu na visaidizi kwa ajili ya wanafunzi wenye ulemavu wanaosoma katika shule za misingi na sekondari nchini. Sambamba na mikakati hiyo, Serikali kupitia Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu imekuwa ikitoa kipaumbele katika kutoa mikopo kwa wanafunzi wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutumia fursa hii kupitia Bunge lako Tukufu kuwakumbusha wale wote wanaojenga majengo maalum yakiwemo ya maghorofa kuweka miundombinu rafiki ili kuwawezesha wanafunzi wenye ulemavu kupata huduma za kielimu pasipo vikwazo.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, nawaomba Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuhamasisha jamii kushirikiana na Serikali katika kujenga mazingira rafiki ya utoaji wa elimu kwa wanafunzi wenye ulemavu.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Sera ya Elimu inasema mlinganyo wa vyoo kwa wanafunzi wa kike uwe choo kimoja kwa wasichana 20 na choo kimoja kwa wavulana 25:-
Je, utekelezaji wa Sera hiyo kwenye eneo hili ukoje?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MTAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali ya sasa kuna uwiano wa choo kimoja kwa wanafunzi wa kike katika shule za msingi ni 52 na wavulana ni 54. Kwa upande wa shule za sekondari uwiano ni wanafunzi 23 kwa choo kimoja kwa wasichana na wavulana ni 25.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imetenga shilingi bilioni 12.9 kwa ajili ya ujenzi wa matundu ya vyoo 8,791 kwa shule za msingi na matundu 1,942 kwa shule za sekondari. Kazi hiyo inafanywa na Serikali kwa kushirikisha nguvu za wananchi na wadau mbalimbali wa maendeleo. Azma ya Serikali ni kuhakikisha miundombinu ya vyoo inajengwa ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia mashuleni.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Wakazi wanaoishi katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro wamekatazwa kulima kwenye maeneo wanayoishi kwa mujibu wa sheria hali iliyochangia wakazi wengi katika eneo hilo ambao ni wafugaji kukabiliwa na njaa pamoja na umaskini mkubwa wa kipato:-
Je, ni lini Serikali itarekebisha Sheria ya Mamlaka ya Hifadhi (Ngorongoro Conservation Area Act), 1959 Revised Edition, 2002) ili wananchi wa maeneo haya wapate maeneo kwa ajili ya shughuli zao za kilimo na ufugaji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kwa mujibu wa sheria iliyoanzisha Hifadhi ya Ngorongoro, Sheria ya Kuhifadhi Eneo la Ngorongoro ya mwaka 1959 iliyopitiwa mwaka 2002 (The Ngorongoro Conservation Area Act 1959, R.E 2002) wananchi wakaazi katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro hawaruhusiwi kulima bali kufuga peke yake.
Mheshimiwa Spika, kutokana na zuio la kisheria la kulima, wakazi wa eneo la Ngorongoro ambao kwa asili yao ni wafugaji, wamekuwa wakitengewa bajeti ya kununulia mahindi ambapo takribani tani 3,600 hugawiwa bila malipo kila mwaka kwa matumizi ya chakula hususan kwa wale uwezo, mahindi hayo huuzwa kwao kwa bei pungufu ya bei ya soko.
Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na changamoto ya chakula, mnamo mwaka 2007, mamlaka ilianza mchakato wa kupata maeneo ya kilimo nje ya hifadhi kwa kutenga bajeti na kuwezesha mradi wa JEMA. Malengo mawili ya mradi wa JEMA ulioko katika Kata ya Oldonyosambu ni haya yafuatayo:-
(a) Kuwaondoa wahamiaji walioingia ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro ambao hawakuwa wakazi halali kwa kuzingatia kwamba wakazi halali ni wale waliokuwepo pamoja na uzao wao wakati eneo la Hifadhi ya Ngorongoro lilipotangazwa rasmi mwaka 1959.
(b) Kutoa fursa kwa wakazi wenyeji na halali ambao wangependa kufanya shughuli za kilimo na ufugaji nje ya hifadhi.
Mheshimiwa Spika, pamoja na mradi huu kuendelea, tathmini ya awali inaonesha upungufu kwa baadhi ya waliohamishiwa eneo la mradi kuuza maeneo waliyopewa na kurejea kinyemela ndani ya hifadhi. Kutokana na upungufu huo, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kushirikiana na uongozi wa Wilaya ya Ngorongoro, inaendelea kuchukua hatua ya kuzuia uuzwaji wa maeneo katika eneo la mradi.
Aidha, kwa kuwa maeneo yaliyopatikana hapo awali hayakuweza kutosheleza mahitaji, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kushirikiana na wadau wengine inaendelea kutafuta maeneo mengine yatakayotumika kwa kilimo.
Mheshimiwa Spika, sheria iliyoanzisha eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ilianza kutumika zaidi ya miaka 50 iliyopita na Serikali iko kwenye maandalizi ya awali ya kufanya marekebisho yake. Ni muhimu kuzingatia kwamba, katika marekebisho hayo Serikali itaweka msisitizo zaidi katika kuboresha shughuli za uhifadhi wa eneo la Ngorongoro ili libakie katika orodha ya maeneo ya urithi wa dunia.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Masuala ya watu wenye ulemavu kwa kiasi kikubwa yanazungumzwa na kushughulikiwa katika maeneo ya mijini na kusahau maeneo ya pembezoni ambapo kuna watu wa jamii hiyo.
Je, Serikali ina mpango gani kuhusu watu wenye ulemavu waishio vijijini ambapo matatizo yao ni mengi na makubwa kulingana na jamii inayowazunguka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mhesimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu waishio vijijini, kwa kutambua hilo Serikali imefanya ugatuaji wa shughuli zinazohusu watu wenye ulemavu kwenda katika Serikali za Mitaa. Serikali inaendelea kuzijengea uwezo Halmashauri na watoa huduma
wengine ili kutatua kero zinazowakabili watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kulingana na Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Namba 9 ya mwaka 2010, imeelekeza kuanzisha Kamati za Baraza la Huduma na Ushauri kwa Watu Wenye Ulemavu kuanzia ngazi ya kijiji/ mtaa hadi ngazi ya taifa, ambazo zitasaidia utoaji huduma kwa watu wenye ulemavu. Katika kusimamia utekelezaji wa matakwa ya sheria hii, Serikali imewaagiza Makatibu Tawala wote wa Mikoa kusimamia uanzishwaji wa Kamati za Mikoa, Halmashauri, Kata na Vijiji kutoa huduma kwa watu wenye ulemavu maana ndiko walipo watu wengi wenye ulemavu.
Mheshimiwa Spika, naomba nitoe rai kwa jamii kuanzisha vyama vya kiraia vikiwemo Vyama vya Watu wenye Ulemavu ambavyo vimekuwa vikifanya kazi kwa ukaribu na wenye ulemavu hadi vijijini.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Haki ya kupata taarifa ni haki ya msingi kwa kila Mtanzania na vyombo vyetu vya habari havina wakalimani wa lugha ya alama kwa ajili ya kuwawezesha viziwi kupata habari kwa uelewa uliotimilifu kama raia wengine.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa vyombo vya habari hasa tv vinaajiri wakalimani hasa katika taarifa za habari ili waweze kufuatilia matukio yanayooneshwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Amina Saleh Mollel (Mbunge), kwa kuona umuhimu wa suala hili pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote hasa Mheshimiwa Stella Alex Ikupa (Mbunge) ambaye naye aliuliza swali hili tarehe 08/05/2017 katika mjadala wa bajeti ya Wizara yetu.
Napenda kulitaarifu Bunge lako kuwa baada ya swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa Mbunge, Wizara iliitisha kikao cha wadau mbalimbali wakiwepo Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, VETA, Chama cha Wakalimani wa Lugha za Alama (TASLI), TBC na wadau wengine ili kutafakari namna ya kutekeleza kwa haraka azma hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mengine, tulikubaliana kwamba VETA watoe mafunzo hayo kwa kushirikiana na CHAVITA na TASLI, kutokana na mtandao mkubwa ambao VETA wanao na VETA wamekubali. TASLI wamepewa kazi ya kuandaa kanzi data za wakalimani wa lugha ya alama kwa viziwi, na TCRA wanaandaa kalenda yaani road map ya utekelezaji wa matumizi ya huduma za wakalimani wa lugha ya alama katika vituo vya televisheni nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na hatua hizo TBC inaendelea na mawasiliano yake na Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Sebastian Kolowa - Taasisi ya Elimu ya Juu, inayofundisha wataalamu wa lugha ya alama kuona ni namna gani shirika linavyoweza kuwatumia wataalamu, wahitimu na wanafunzi wa chuo hicho kutoa kwa muda huduma ya lugha ya alama kupitia TBC.
Aidha, Serikali imeandaa kutekeleza suala hili kwa kuweka wakalimani wa lugha ya alama katika matukio ya Kitaifa kama maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano yaliyofanyika 26 Aprili, 2017. Vilevile TBC iko kwenye mchakato wa kuajiri wakalimani wachache kwa kuanzia wa lugha za alama kwa taarifa zake za habari na katika matangazo machache yanayorushwa na televisheni hiyo ya TBC.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa wito kwa wamiliki wa vyombo vya habari binafsi nchini nao kuanza mchakato wa kuwaajiri wakalimani wa lugha ya alama ili waweze kuwawezesha watu wa kundi hili kupata taarifa kupitia vyombo vyao habari.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Mkataba wa Kimataifa kuhusu haki za watu wenye ulemavu (UNCRPD) wa mwaka 2006 Ibara ya tisa (9) unazungumzia haki za watu wenye ulemavu kupata habari kwa kuwa kumekuwa na changamoto za kisheria hususani katika nyaraka zenye hati miliki:-
Je, ni lini Serikali itaridhia Mkataba wa Kimataifa wa mwaka 2013 Marrakesh Treaty ambao unalenga kuondoa vikwazo mbalimbali vinavyozuia walemavu wasioona waweze kupata habari katika mifumo inayokidhi mahitaji yao?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkataba wa Marrakesh ni mkataba wenye lengo la kuwawezesha watu wenye matatizo ya kuona, kupata nakala za maandishi yenye hati miliki na vifaa vya kuwasaidia kuweza kupata elimu kwa urahisi kwa kutumia vitabu, magazeti, burudani na shughuli mbalimbali za kijamii, hivyo kuwasaidia katika maisha yao ya kila siku na kuwawezesha kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiuchumi na kuondoa umaskini hatimaye kuchangia katika pato la Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania kupitia COSOTA ilisaini itifaki ya Marrakesh tarehe 28 Juni, 2013. Wizara inaandaa mapendekezo ya kuridhia Itifaki ya Marrakesh kulingana na taratibu zinavyoelekeza na hivi sasa inakusanya maoni ya wadau kuhusu mkataba huo. Baada ya kukamilika kwa hatua hiyo, waraka wa mapendekezo utawasilishwa Baraza la Mawaziri na hatimae kuletwa Bungeni kwa lengo la kuridhia.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Wizara ni kuleta Itifaki ya Marrakesh Bungeni haraka iwezekanavyo mara baada ya kukamilisha taratibu zinazotakiwa kufuatwa ili kuridhia Mkataba wa Kimataifa.(Makofi)
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Haki ya kupata taarifa ni haki ya msingi kwa kila Mtanzania na vyombo vyetu vya habari havina wakalimani wa lugha ya alama kwa ajili ya kuwawezesha viziwi kupata habari kwa uelewa uliotimilifu kama raia wengine.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa vyombo vya habari hasa tv vinaajiri wakalimani hasa katika taarifa za habari ili waweze kufuatilia matukio yanayooneshwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Amina Saleh Mollel (Mbunge), kwa kuona umuhimu wa suala hili pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote hasa Mheshimiwa Stella Alex Ikupa (Mbunge) ambaye naye aliuliza swali hili tarehe 08/05/2017 katika mjadala wa bajeti ya Wizara yetu.
Napenda kulitaarifu Bunge lako kuwa baada ya swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa Mbunge, Wizara iliitisha kikao cha wadau mbalimbali wakiwepo Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, VETA, Chama cha Wakalimani wa Lugha za Alama (TASLI), TBC na wadau wengine ili kutafakari namna ya kutekeleza kwa haraka azma hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mengine, tulikubaliana kwamba VETA watoe mafunzo hayo kwa kushirikiana na CHAVITA na TASLI, kutokana na mtandao mkubwa ambao VETA wanao na VETA wamekubali. TASLI wamepewa kazi ya kuandaa kanzi data za wakalimani wa lugha ya alama kwa viziwi, na TCRA wanaandaa kalenda yaani road map ya utekelezaji wa matumizi ya huduma za wakalimani wa lugha ya alama katika vituo vya televisheni nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na hatua hizo TBC inaendelea na mawasiliano yake na Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Sebastian Kolowa - Taasisi ya Elimu ya Juu, inayofundisha wataalamu wa lugha ya alama kuona ni namna gani shirika linavyoweza kuwatumia wataalamu, wahitimu na wanafunzi wa chuo hicho kutoa kwa muda huduma ya lugha ya alama kupitia TBC.
Aidha, Serikali imeandaa kutekeleza suala hili kwa kuweka wakalimani wa lugha ya alama katika matukio ya Kitaifa kama maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano yaliyofanyika 26 Aprili, 2017. Vilevile TBC iko kwenye mchakato wa kuajiri wakalimani wachache kwa kuanzia wa lugha za alama kwa taarifa zake za habari na katika matangazo machache yanayorushwa na televisheni hiyo ya TBC.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa wito kwa wamiliki wa vyombo vya habari binafsi nchini nao kuanza mchakato wa kuwaajiri wakalimani wa lugha ya alama ili waweze kuwawezesha watu wa kundi hili kupata taarifa kupitia vyombo vyao habari.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Utekaji nyara na mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino) vilikithiri kwenye miaka ya 2000 hali iliyopelekea Serikali kuanzisha kambi maalum kwa ajili ya usalama wao.
(a) Je, Serikali imeanzisha kambi ngapi mpaka sasa na ni katika Mikoa na Wilaya zipi?
(b) Je, ni watu wangapi wenye ulemavu wa ngozi wanaoishi katika makambi hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WATU WENYE ULEMAVU (MHE. STELLA A. IKUPA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b)kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna kambi iliyoanzishwa na Serikali kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa ngozi hadi sasa, isipokuwa kuna shule katika baadhi ya Mikoa kama vile Shule ya Buhangija iliyoko Mkoani Shinyanga ambayo imepokea watoto wenye ulemavu wa ngozi kwa kuletwa na wazazi, viongozi wa vijiji, Maofisa Ustawi wa Jamii na Polisi. Hii yote ni katika kunusuru uhai wao, kwani Sera ya Taifa ya watu wenye Ulemavu ya mwaka 2004 inakataza watu kuishi kwenye Kambi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la (b) jibu ni kwamba idadi ya watu wenye ulemavu wa ngozi waishio kwenye Shule ya Buhangija ni 309 ambapo wanaume ni 152 na wanawake ni 157.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Je, ni kwa kiwango gani Serikali imetekeleza agizo la Bunge la kukusanya kodi katika huduma za mahoteli kwenye Hifadhi za Taifa kwa njia ya Concession Fee Fixed Rate?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukusanyaji wa Tozo ya Concession Fees kwa utaratibu mpya wa Fixed Rate ulianza kutekelezwa tarehe 1 Julai, 2017 kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na.234 la mwaka 2017. Kwa mujibu wa Tangazo hilo, kila mgeni anatozwa kati ya Dola za Kimarekani 25 na 50 kulingana na hadhi ya hifadhi husika. Kwa mfano, Hifadhi ya Taifa ya Mikumi ni Dola za Kimarekani 25 na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ni Dola 50 za Kimarekani. Kwa hivi sasa wawekezaji wote wanalipa tozo hiyo kwa viwango vilivyoainishwa katika Tangazo hilo la Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiasi cha Tozo ya Concession Fees kilichokusanywa katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Machi, 2020 kwa mwaka wa fedha 2017/2018 ni shilingi bilioni
18.8 ikilinganishwa na shilingi bilioni 6.9 iliyokusanywa katika kipindi hicho mwaka 2016/2017. Hili ni ongezeko la shilingi bilioni 11.9 ambazo ni sawa na 174%.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyokusanywa kutoka katika makusanyo ya Tozo ya Concession Fees kwa kipindi hicho ni shilingi bilioni 3.4 ikilinganishwa na kipindi kama hicho cha mwaka wa fedha 2016/2017 ambapo jumla ya shilingi bilioni 1.2 zilikusanywa na kupelekwa TRA.
MHE. HAWA M. CHAKOMA (K.n.y. MHE. AMINA S. MOLLEL) aliuliza:-
Baadhi ya mila na tamaduni katika jamii za wafugaji hapa nchini haziwapeleki watoto wa kike shule, badala yake wanawaozesha katika umri mdogo kinyume na ridhaa yao, hivyo kukiuka sheria za nchi.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kuwa mila na tamaduni hizo haziwanyimi watoto wa kike haki yao ya kupata elimu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua haki za msingi za mtoto ikiwemo ya kupata elimu na kuendelezwa ili kupata nguvu kazi yenye tija itakayochangia kujenga uchumi unaotarajiwa katika nchi yetu. Serikali imechukua hatua mbalimbali kuhakikisha kuwa mila na tamaduni zenye madhara zinazosababisha watoto kushindwa kwenda shule zinashughulikiwa ipasavyo. Utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya Mtoto ya mwaka 2008 inayoelekeza kutoa haki kwa mtoto bila kubaguliwa ikiwemo kuendelezwa kielimu na kutokomeza mila zinazoruhusu ndoa katika umri mdogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekezaji wa Sheria Namba 21 ya mwaka 2009 inayoelekeza utoaji wa haki na huduma ya msingi kwa mtoto ikiwemo elimu, malazi na huduma ya afya na utekelezaji wa Mpango wa Kazi wa Kitaifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto wa mwaka 2017/2018 ambao utaisha mwaka 2021/2022 ambao umelenga kushirikisha jamii kutokomeza mila na tamaduni zenye madhara kwa watoto na hasa watoto wa kike ili kumuwezesha kupata haki zake za msingi ikiwemo elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2017/2018 Wizara imetoa elimu kuhusu mila na desturi zenye madhara, ikiwemo ukeketaji, mimba na ndoa za utotoni kwa jumla ya wananchi 13,020 yakiwemo makundi mbalimbali ya mangariba, viongozi wa jadi na jamii ya wafugaji katika Mikoa ya Dodoma, Arusha, Mara, Shinyanga, Tabora, Lindi, Tanga, Dar es Salaam na Katavi. Aidha, Wizara imeandaa mdahalo mkubwa wa Kitaifa mwezi Oktoba mwaka huu utakaojumuisha wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na viongozi wa kisiasa, viongozi wa dini na viongozi wa kimila ili kujadili na kupata muafaka wa Kitaifa wa namna ya kutokomeza matatizo ya ukatili kwa watoto yakiwemo ukeketaji, ndoa na mimba za uototoni, ambayo yamekuwa yakiongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara pia, imeanzisha klabu za watoto na mabaraza ya watoto na kamati za ulinzi wa wanawake na watoto katika ngazi mbalimbali za utendaji kuanzia ngazi ya taifa hadi kijiji ili kujadili na kutafuta ufumbuzi wa masuala ya ukatili wa wanawake na watoto, yakiwemo masuala ya mila na tamaduni zenye madhara kwa watoto.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-
Mfuko wa Watu wenye Ulemavu ulianzishwa kwa Sheria Na.9 ya mwaka 2010 na lengo la mfuko huo ni kusaidia Baraza la Watu Wenye Ulemavu kufanya kazi zake kwa ufanisi, kuendesha tafiti mbalimbali na kubaini changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu. Hata hivyo mfuko huo haukutengewa fedha katika bajeti ya mwaka 2016/2017.
Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya mfuko huo ili uweze kufanya kazi zake kwa ufanisi kama ilivyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WATU WENYE NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI ULEMAVU (MHE. STELLA I. ALEX) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Watu wenye Ulemavu umeanzishwa kwa mujibu wa kifungu cha 57(1) cha Sheria ya Watu wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa lengo la kuwezesha utekelezaji wa majukumu ya Baraza la Taifa la Ushauri kwa Watu wenye Ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza matakwa ya sheria hii, Serikali ilizindua rasmi Baraza la Ushauri la Taifa kwa Watu wenye Ulemavu mnamo Novemba, 2014 ambalo limejumuisha Wizara zinazohusika na masuala ya watu wenye ulemavu, Vyama vya Watu wenye Ulemavu, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Chama cha Wafanyakazi. Aidha, kupitia Serikali ya Awamu ya Tano Baraza limeanza Rasmi kazi na Serikali imekuwa ikitenga bajeti kila mwaka kwa ajili ya uendeshaji wa vikao ambavyo kwa mujibu wa sheria vinafanyika vinne kwa mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mchakato wa kuwa na Baraza la Taifa la Ushauri kwa Watu wenye Ulemavu umeshakamilika, Serikali kupitia bajeti ya mwaka 2018/2019 imetenga fedha kwa ajili ya uanzishwaji wa Mfuko wa Watu Wenye Ulemavu.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-

Tatizo la kukosekana kwa mafuta yanayosaidia kukinga ngozi dhidi ya mionzi kwa watu wenye Ulemavu wa ngozi hapa nchini limekuwa kubwa na hivyo kuwa chanzo cha magonjwa ya saratani kwa watu hao na kusababisha vifo. Inakadiriwa kuwa asilimia 70 hadi 75 ya vifo vya watu wenye ulemavu wa ngozi vinatokana na saratani.

Je, ni lini Serikali itatoa huduma hiyo bure kwa watu wenye ulemavu wa ngozi katika maeneo yote nchini kama inavyotoa dawa za kufubaza virusi kwa watu wenye maambukizi ya UKIMWI?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika kwa niaba ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto inatambua uwepo wa watoto wenye ulemavu wa ngozi kwa maana albinos (albinism) nchini na umuhimu wa wao kupata mafuta hayo ili kuwasaidia kukinga ngozi yao dhidi ya mionzi. Kwa kutambua umuhimu wa mafuta hayo, kwa jina la kitaalam tunaita Sun Protection Factor 30, Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto kuanzia mwaka 2013 iliingiza mafuta hayo kwenye orodha ya Taifa ya dawa muhimu ili ziweze kununuliwa kutunzwa na kusambazwa na Bohari ya Dawa nchini kote.

Aidha, Bohari ya dawa tangu mwaka 2015 imekuwa ikinunua mafuta hayo kadri ya maombi yalivyowasilishwa na vituo vya kutolea huduma ya afya. Baadhi ya taasisi kama vile Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Hospitali ya Mirembe
- Dodoma, Hospitali ya Kisarawe na Ilemela zilipata mafuta haya kutoka MSD.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa hali ya ualbino ni hali ya kudumu na hivyo kuangukia katika kundi la magonjwa sugu, ambapo Sera ya Afya mwaka ya 2007 inatamka wazi kuwa kundi hili litapata huduma bure, hivyo basi, nitoe rai kwa hospitali na vituo vyote vya kutolea huduma za afya katika mikoa ya Halmashauri kuingiza bajeti ya mafuta hayo katika mipango yao ili iweze kuagiza mafuta hayo kutoka bohari ya dawa.
Aidha, Wizara itaendelea kuhamasisha wazalishaji wa ndani ya nchi wa mafuta hayo katika kiwanda kilichopo katika Hospitali ya KCMC.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-

Kuna taarifa kwamba nchi ya Kenya inatarajia kutekeleza mpango wa kujenga mabwawa makubwa kwa ajili ya uzalishaji umeme. Kwa kuwa ujenzi huo unatishia ustawi wa uwepo wa Hifadhi ya Taifa Serengeti. Je, Serikali ya Tanzania inachukua hatua gani kuhusu mpango huo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maluum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 Serikali ilipata taarifa ya mpango wa ujenzi wa mabwawa ya umeme uliopangwa kutekelezwa na Serikali ya Kenya. Wizara ilifanya uchunguzi wa madhara yatakayosababishwa na miradi hiyo katika Hifadhi ya Taifa Serengeti kwa kukusanya takwimu za mtiririko wa maji na kulinganisha na mahitaji halisi ya miradi iliyotarajiwa. Uchunguzi ulibaini kuwa utekelezaji wa miradi hiyo, ungesababisha athari kubwa ya kiikolojia ya Serengeti kwani takwimu zilizotumiwa na wataalam wa nchini Kenya kuhalalisha mradi huo hazikuwa sahihi. Miongoni mwa athari hizo ni pamoja na kuhatarisha ustawi wa maisha ya viumbe hai kutokana na ukosefu wa maji katika Mto Mara wakati wa kiangazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya Mto Mara yanajadiliwa na Tume ya kuratibu Bonde la Ziwa Victoria (Lake Victoria Basin Commission) chini ya Wizara ya Mambo Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Aidha, majadiliano mbalimbali kuhusu hatima ya Mto Mara au miradi inayoathiri maji ya Mto Mara ikiwemo ujenzi wa Bwawa la Umeme la Ewaso, Ngiro nchini Kenya yanaendelea kujadiliwa katika mpango wa Bonde la Mto Mara uliosainiwa mwezi Septemba, 2016 chini ya Wizara ya Maji. Katika pango huo suala la athari za ujenzi mabwawa kwa maliasili zitakazoathirika kutokana miradi itakayofanyika nchini Kenya na Tanzania limejadiliwa na mapendekezo kutolewa kuhusu namna ya kukabiliana na matumizi yenye utata.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-

Je, ni kwa namna gani Wakala wa Misitu (TFS) inashirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa, hususan Wilaya katika kusimamia misitu hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Taarifa ya Tathmini ya Rasilimali za Misitu Tanzania (National Forest Resources Monitoring and Assessment - NAFORMA) ya mwaka 2015, Tanzania ina rasilimali za misitu zinazokadiriwa kufikia hekta milioni 48.1 ambapo asilimia 34 inasimamiwa na Serikali Kuu, asilimia 6.5 inasimamiwa na Halmashauri, asilimia 45.7 inasimamiwa na vijiji, asilimia 7.3 inasimamiwa na Sekta Binafsi na asilimia 6.0 ya misitu iko katika ardhi huria (general land). Kulingana na taratibu za Serikali, misitu ya Tanzania inasimamiwa kwa mujibu wa Sheria ya Misitu Na. 14 ya Mwaka 2002.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria hiyo, Mamlaka za Usimamizi wa Misitu Nchini zipo katika Wizara mbili, nayo ni Wizara ya Maliasili na Utalii ambayo imekasimu mamlaka hayo kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) ambapo una jukumu la kusimamia misitu ya Hifadhi ya Serikali Kuu na misitu mingine yote ambayo haijahifadhiwa kisheria; na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) inayosimamia misitu iliyopo chini ya Mamlaka za Serikali za Mitaa (Halmashauri na Vijiji).

Mheshimiwa Spika, kwa tafiti zilizopo, misitu ya Tanzania inakabiliwa na changamoto kubwa mbili; kwanza, uharibifu mkubwa wa misitu ambao kwa sasa umefikia kiasi cha hekta 470,000 kwa mwaka; na pili, mahitaji ya mazao ya misitu yanayozidi uwezo wa misitu kwa zaidi ya meta za ujazo millioni 19.5. Ili kukabiliana na changamoto hizo, Serikali imeendelea kufanya jitihada za pamoja kati ya Wizara hizi mbili zinazosimamia rasilimali za misitu. Kupitia ushirikiano huo, Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia taasisi yake ya TFS imekuwa ikishirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kutatua changamoto hizo.

Mheshimiwa Spika, kupitia mpango huo wa pamoja, Wizara ya Maliasili na Utalii na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa tumekubaliana kushirikiana katika maeneo mbalimbali ambayo ni pamoja na kuimarisha usimamizi wa misitu na ufuatiliaji wa miradi inayofadhiliwa na Mfuko wa Misitu Tanzania. Ushirikiano huo unashirikisha ngazi ya wilaya ambapo Mwenyekiti wa Kamati ya Uvunaji wa Mazao ya Misitu katika Wilaya ni Mkuu wa Wilaya.

Mheshimiwa Spika, aidha, Afisa Misitu wa Halmashauri ya Wilaya ni Mjumbe wa Vikao vya Uvunaji na ndiye anayetoa leseni za uvunaji wa mazao ya misitu katika Wilaya husika. Vilevile, ushirikiano mwingine upo katika kutoa elimu kwa Umma, kuhifadhi misitu kwa njia shirikishi, kuanzisha magulio ya mkaa na kusimamia doria za kudhibiti uvunaji na usafirishaji haramu wa mazao na bidhaa za misitu.

Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha ushirikiano huo, tarehe 26 Mei, 2016 Wizara ya Maliasili na Utalii ilisaini Mkataba wa Makubaliano na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ya kuimarisha zaidi ushirikiano katika usimamizi wa misitu nchini na utawala bora. Kufuatia makubaliano hayo, vikao vya pamoja katika ngazi ya wilaya vya kujadili utekelezaji vimekuwa vikifanyika kila mwaka ili kuchambua changamoto mbalimbali.

Mheshiwa Spika, kwa ujumla utunzaji na uendelezaji wa misitu nchini unakabiliwa na changamoto mbalimbali kulingana na mazingira ya mikoa na wilaya husika.

Hata hivyo, Serikali kupitia Wizara hizi mbili itaendelea kuweka mikakati mbalimbali ili kuwezesha rasilimali za misitu kuendelea kutumika kwa kufuata taratibu zilizopo ili rasilimali hizo zinufaishe vizazi vya sasa na vijavyo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. PROF. JUMANNE A. MAGHEMBE (MHE. AMINA S. MOLLEL) aliuliza:-

Shule ya Viziwi Mwanga hutoa Elimu ya Msingi kwa Watoto wasiosikia na wasioongea kwa Mikoa ya Kilimanjaro, Tanga na Arusha; wanapohitimu Elimu ya Msingi, Wanafunzi hao hujiunga na Shule za Sekondari za kawaida ambazo hazina Walimu wenye Taaluma Maalum, vifaa na mazingira rafiki kwa Watoto wenye ulemavu:-

Je, ni lini Serikali itajenga Shule ya Sekondari Maalum kwa Watoto Viziwi (wasiosikia na wasioongea)?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prof. Jumanne Abdallah Maghembe Mbunge wa Mwanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu kwa wanafunzi viziwi inatolewa katika Shule maalum 17 za Msingi na vitengo maalum 120. Shule hizi za Msingi zina jumla ya wanafunzi 7,212 na jumla ya walimu 885 wataalam wa kufundisha wanafunzi viziwi. Vilevile, ipo Shule maalum moja ya Sekondari na vitengo maalum 23 vya sekondari. Shule hizi za sekondari zina jumla ya wanafunzi viziwi 1,778 na jumla ya walimu 302 wataalam wa kufundisha wanafunzi viziwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekamilisha ujenzi wa Shule ya Sekondari Maalum ya Viziwi iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Meru katika eneo la Tengeru (Patandi), ambayo mwaka 2020 kwa mara ya kwanza itaanza kudahili wanafunzi viziwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kutoa wito kwa wadau wote wa elimu wenye nia ya kujenga Shule za Watoto wenye ulemavu wakiwemo viziwi, wafanye hivyo, Serikali itatoa vibali husika kwa kuzingatia taratibu na sheria husika.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-

ATM za Benki nyingi hapa nchini hazikidhi mahitaji ya watu wenye ulemavu:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa ATM za Benki zinawekewa mifumo inayokidhi mahitaji ya watu wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tangu Serikali ilipoanza maboresho ya mifumo ya malipo nchini mwaka 1996, Benki Kuu ya Tanzania imeendelea kusimamia usimikaji wa mifumo ya kisasa, mahiri na salama ili kuendana na mahitaji ya soko na mabadiliko ya teknolojia. Maboresho hayo ya mifumo yanalenga pamoja na mambo mengine kukidhi mahitaji ya makundi mbalimbali katika jamii wakiwemo watu wenye mahitaji maalum, hususan walemavu.

Mheshimiwa Spika, Mei, 2017 Benki Kuu ya Tanzania ilitoa mwongozo wa mfumo wa malipo kwa njia ya mtandao ikiwa ni mpango wa Serikali wa kuhakikisha kuwa huduma za malipo kwa njia ya mtandao yanafanyika kwa usalama na kukidhi mahitaji ya makundi yote katika jamii. Miongoni mwa vipengele muhimu na nyeti, hususan kwa watu wenye ulemavu vilivyoainishwa kwenye mwongozo huo ni alama za utambuzi, usalama wa mifumo na uwezo wa mifumo wa kutunza siri za wateja. Pamoja na Serikali kutoa mwongozo huo, benki zetu zote hapa nchini hazijafanikiwa kusimika ATM maalum na rafiki kwa watu wenye ulemavu, hususan watu wenye ulemavu wa macho. Hii ni kutokana na ukweli kwamba teknolojia ya ATM kwa watu wenye ulemavu wa macho ni ngeni na pia ina mfumo au mahitaji ya ziada ikilinganishwa na ATM za kawaida.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya uduni wa baadhi ya miundombinu kwa watu wenye ulemavu, hususan walemavu wa miguu imetatuliwa kwa sehemu kubwa na hivyo kuwa rafiki katika maeneo mengi yanayotoa huduma za kibenki kwa kutumia mashine za ATM. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa Serikali itaendelea kufuatilia kwa karibu suala hili ili kuhakikisha kuwa mifumo ya miamala kwa njia ya ATM inakuwa rafiki kwa makundi yote wakiwemo watu wenye ulemavu.
MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-

Je, Serikali imejipangaje kutekeleza mojawapo ya malengo katika Mpango wa Maendeleo wa miaka 5 kwa Taifa 2016/2017, 2020/2021 katika kupanua wigo wa Utalii nchi (diversification)?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kupanua wigo wa mazao ya utalii, Wizara kwa kushirikiana na wadau wa utalii inaendelea na jitihada za kuendeleza mazao mbalimbali ya utalii na kutangaza ikiwemo; kuanzisha mradi wa utalii wa utamaduni kwenye maeneo mbalimbali nchini; utalii wa fukwe kwa kuanzisha kurugenzi itakayosimamia uendelezaji wa utalii huo nchini; utalii wamali kale kwa kuimarisha vitu mbalimbali vya mali kale, pamoja na kuimarisha utalii wa mikutano na maonesho (Meetings Incentives Conference and Events-) kwa kuboresha muundo wa Bodi ya Utali(TTB) utakaowezesha kuwa na kitengo kinachosimamia utalii huo, pamoja na kufanya tathmini ya ujenzi wa kumbi za mikutano katika eneo la Pwani la Bagamoyo na Dar es Salaam, na utalii wa meli kubwa za kitalii (Cruiseship Tourism) ambapo tunashirikiana na Mamlaka ya Bandari kuboresha miundombinu ya bandari ili kukidhi mahitaji ya utalii huo nchini pamoja na kuendeleza utalii wa Jiolojia katika Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, Wizara imeanzisha shughuli mpya za utalii zikiwemo; safari za puto (Hot air balloon) katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha; utalii wa kutembea katika kamba(canopy walkway) katika Hifadhi ya Taifa Manyara; Utalii wa kuzoesha Sokwe (habituated chimpamzees) katika Hifadhi ya Taifa ya Rubondo pamoja na kuimarisha na kutangaza Hifadhi za Misitu ya Asili nchini ili kuvutia watalii kutembelea maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeanza kutekeleza Mradi wa Resilient Natural Resource Management for Tourism and Growth (REGROW) ambao kazi zake ni kuendeleza na kutangaza vivutio vya utalii, kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika Sekta ya Utalii pamoja na kuboresha miundombinu inayozunguka katika vivutio vya utalii vilivyopo Nyanda za Juu Kusini ikiwemo barabara na viwanja vya ndege. Ni imani yangu kuwa, utekelezaji wa mradi huu utasaidia ukuaji wa Sekta ya Utalii katika Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini sambamba na kupanua wigo wa mazao ya utalii katika utalii katika Ukanda wote wa Kusini kwa ujumla.