Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Anastazia James Wambura (29 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Pongezi nyingi kwa Waziri na Naibu wake kwa hotuba nzuri na kwa kazi nzuri hasa ya kusuluhisha migogoro ya wakulima na wafugaji.
Kwanza naomba Wizara yako ifuatilie tozo wanayotozwa wavuvi wa Mtwara, shilingi mia tano arobaini na saba kwa kilo ya samaki. Je, ni tozo ya watu binafsi? Kimsingi tozo hii imeathiri uchumi wa wavuvi wa Mtwara na naomba Mheshimiwa Waziri atembelee Mkoa wa Mtwara kama alivyofanya kwa jamii za wakulima na wafugaji.
Pili, napongeza jinsi Wizara ilivyoongeza eneo la kilimo cha umwagiliaji katika nchi yetu. Umwagiliaji huu kwa kiasi kikubwa ni kwa mazao ya chakula cha wanga. Ushauri wangu kwa Wizara ni kuongeza uzalishaji wa mbogamboga na matunda kwa kuwezesha umwagiliaji wa matone (Drip Irrigation).
Hoja yangu inatokana na hali halisi ya upatikanaji wa mboga na matunda kwa msimu fulani ambapo wakati mwingine bidhaa hizi huadimika na kupelekea bei kupanda kwa kiasi kikubwa. Athari za hali hii zinaweza kuonekana katika lishe ya jamii kuwa duni. Hivyo, naomba wataalam wa Wizara wajitahidi kuwaandaa wananchi pale watakapopata mikopo ya milioni hamsini wengine wawekeze kwenye kilimo cha mbogamboga na matunda kwa (Drip irrigation).
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. „Kama mnataka mali mtaipata shambani‟
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri Mahiga, Naibu Waziri Kolimba na timu yote ya Watendaji kwa kuandaa vizuri hotuba ya bajeti ya Wizara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri katika maeneo mawili. Kwanza, nashauri Wizara iwekeze katika viwanja vilivyoko nje ili kupata fedha za kuendesha balozi zetu. Kwa mfano, kiwanja tulichopewa na Serikali ya Msumbiji tukakiacha, mwisho wake tunaweza kunyang‟anywa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Maafisa wa Korea Kusini waliwahi kuja kuongea na Kamati yetu ya Mambo ya Nje na kuialika iende nchini humo ili kuona uwezekano wa kuanzisha Ofisi ya Ubalozi Korea Kusini. Ni ushauri wangu kwamba Wizara ilifanyie kazi hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hongera sana kwake Mheshimiwa Waziri Charles Tizeba na Naibu Waziri Mheshimiwa William Olenasha kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na timu yao, Katibu Mkuu na watendaji wa Wizara. Hotuba yao ni nzuri na imejitosheleza kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji lishe bora kwa wananchi wote wa Tanzania. Ni muhimu tuwahakikishie upatikanaji wa mboga na matunda kwa mwaka mzima kwa bei nafuu. Wizara ianzishe Drip Irrigation kila Wilaya kwa kutumia visima virefu. Kilimo hiki pamoja na kuboresha lishe ya jamii kitasadia kuongeza kipato hasa kwa makundi ya wanawake na vijana. Pia kitaongeza ukuaji wa kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri zitembelewe na ukaguzi ufanyike kuhusiana na tozo kubwa wanazotozwa wavuvi. Yapo malalamiko ya kwamba wavuvi kule Mtwara wanalipa dola 500 kwa kila kilo moja ya samaki wanaovuliwa kutoka Msumbiji na hivyo kupelekea hasara kwani bei ya kuuzia huwa ni ya chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hongera sana kwa usimamizi mzuri wa zao la korosho. Kwa msimu huu umakini uongezeke katika ugawaji wa pembejeo kwa wakati na udhibiti wa kangomba. Kutokana na bei nzuri ya korosho ya mwaka uliopita wakulima wengi sasa wanaomba mfumo wa stakabadhi ghalani kwa mazao mengine kama mbaazi. Wizara iangalie uwezekano wa kuanzisha mfumo huu kwa mazao mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na ninaitakia Wizara kila la heri.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Naibu Spika, hongera sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kuandaa vizuri hotuba ya Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepitia majedwali katika kitabu cha hotuba jedwali namba 13 la orodha ya visima vilivyochimbwa hadi mwezi Machi, 2017, sehemu inayoonesha uwezo wa kisima kuna maeneo yameachwa wazi na maeneo mengine yameachwa wazi kwa uzembe. Kwa mfano, kisima namba 204 cha Msijute kilichofadhiliwa na ESRF na kuchimbwa na Wakala wa Visima wa Serikali kuna uzembe mkubwa umefanyika. Baada ya kuchimba kisima waliletwa watu wa kupima uwezo wake wakatoa taarifa kwamba hakuna maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wa ESRF wamehitaji wapate taarifa itakayowaelekeza nini kifanyike ili maji yapatikane lakini miezi imepita bila mafanikio, binafsi wakala waliniambia niongeze shilingi milioni tatu ili wachimbe kisima kingine na baadae mwezi wa nne nikaambiwa niongeze shilingi milioni sita ili nichimbiwe kisima kingine. Ajabu ni kwamba watu wa bonde walipokuja wamepima na kuona kwamba maji yapo kwa asilimia 30 ya mita 150 zilizochimba, wamesema kwamba wale waliojaribu kupima uwezo wa kisima walitumia pump kubwa ambayo ilikausha maji kwa muda mfupi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapendekezo yao ni kwamba zingetumika pump zenye uwezo tofauti na pia ilibidi wa-flash kisima, ushauri wangu kisima kile ni kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa Msijute ambao walimuamini Wakala wa Visima wa Serikali. Ni vema iandikwe taarifa ya ukweli na uwazi kwa ESRF ili aweze kuchukua hatua za ziada kuwasaidia wananchi wa kijiji cha Msijute wapate maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, chunguzeni visima vyote ambavyo havioneshi uwezo wake mjue sababu na taarifa itolewe kuepusha ubabaishaji wa baadhi ya wachimbaji visima. Fikeni katika maeneo husika mkutane na wachimbaji na Mamlaka za Mabonde na wafadhili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa mwisho jioni hii ya leo katika bajeti hii ya Serikali. Nianze kwa kusema naunga mkono hoja. Kabla sijaendelea, napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha na Mipango na Naibu wake Mheshimiwa Masauni pamoja na timu nzima ya Wizara kwa kuandaa vizuri mpango huu. Hata hivyo, Mheshimiwa Waziri alitenda haki katika kuwasilisha. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, sisi Wabunge ni wapika kura wake. Nadhani sote tutakubaliana kwamba hajawaji kutuangusha wapiga kura wake na anazitendea haki kura zetu za ndiyo ambazo tulimpa hapa. Hii ni kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mkuu anafanya kazi bila ya kujali leo ni Jumamosi wala leo ni Jumapili. Kama tutakumbuka ni kwamba juzi tu hapa tarehe 6 Juni, 2021 tulikuwa naye Lindi katika Mkutano wa Wadau wa Korosho na alitoa tamko zuri sana kutoka kwa mama yetu. Kutokana na matamko haya, wakulima na niseme ni wakulima wote wa korosho pamoja na wadau wengine walifarijika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, Jumapili ya tarehe 13 Juni, 2021 tumemwona pia akiwa Singida na Wadau wa Alizeti na ambapo pia alitoa matamko mbalimbali ya kutia faraja kwa wakulima na wadau wa alizeti. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na ninaomba tumwombee kwa Mungu kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia nitoe shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Jenista Mhagama ambaye alichukua swali ambalo aliniulizia mtu kwa niaba tarehe 01 Juni, 2021 linalohusiana na barabara ya kutoka Kibiti – Lindi hadi Mtwara. Hili linazungumzia uharibifu mkubwa wa barabara. Nashukuru sana na ninaomba tu kukumbushia kwamba kweli alifanyie kazi kwa sababu lile ni tatizo kubwa na Serikali ilitoa maelezo hapa kwamba sasa mbadala wake itakuwa ni kwamba magari yenye uzito mkubwa au mizigo mizito iwe inapitia katika Bandari ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo ambalo lipo pale, nafiri inabidi Serikali iliangalie kiupekee zaidi kwa sababu katika maeneo ya Kikula, Kilanjelanje, Mandawa na maeneo mengine, kuna uchimbaji mkubwa wa mawe ambayo yanatumika kama malighafi viwandani kwa ajili ya kutengeneza saruji. Sasa hapa katika haya maeneo utaona kuna uharibifu mkubwa sana, kuna mashimo makubwa ambayo ni hatarishi. Tukisema kwamba mizigo ile iwe inasafirishiwa Bandarini, kule hakuna Bandari ni lazima mizigo hii ipite barabarani kwa ajili ya kupelekwa viwandani. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali iliangalie hili kwa jicho la pekee ili kusudi tuweze kupunguza zile ajali ambazo zinatokea mara kwa mara kutokana na yale mashimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye bajeti sasa. Niseme tu kwa kweli bajeti hii iliyowasilishwa ina ubora wa kipekee ambao hata wachangiaji waliopita wameweza kutaja na kikubwa zaidi ni uendelezaji wa miradi yetu mikubwa ya kimkakati. Kwa sababu hiyo nampongeza sana Mheshimiwa Mheshimiwa Mama Samia Suluhu, Mama yetu mpendwa, Rais wetu pamoja na Makamu wa Rais kwa ujumla na Serikali ya Awamu ya Sita kwa kazi nzuri ambayo wanawafanyia Watanzania. Mungu wetu atusaidie kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ubora wa bajeti hii, ninachokiona kikubwa ni uhitaji zaidi katika kujitegemea. Nasema hivi kwa sababu moja, bado tuna mahitaji makubwa. Tuna mahitaji katika kuendelezaji wa miundombinu mbalimbali katika Sekta ya Afya, sekta ya elimu, sekta ya barabara na kadhalika. Hata hivyo, tuna uhitaji wa kuongeza mishahara kwa Madiwani na kwa Watumishi kwa ujumla kama Mheshimiwa Mama yetu alivyoahidi siku ya Mei Mosi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili ambalo nalisema, la kujitegemea, naomba kurejea maneno ya mpendwa wetu Hayati Mheshimiwa Benjamin William Mkapa ambaye alikuwa ni Rais wa Awamu ya Tatu, alisema maneno yafuatayo, naomba kunukuu: “Napenda kuwakumbusha kuwa njia ya maendeleo imejaa jasho na vumbi. Tuzingatie utamaduni wa kupenda kufanya kazi kwa bidii, maarifa, ubunifu na kujituma. Lawama ni tamu ikitoka mdomoni, lakini peke yake haitapeleka mkono kinywani; na katika kila mfanyakazi akumbuke kuwa muhimu siyo muda anaoutumia kufanya kazi, bali kiasi cha kazi anayoweza kufanya katika muda aliopewa.” mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa hapa mimi niseme ni bidii, maarifa, ubunifu na kujituma. Kimsingi tukiyatekeleza haya, jibu la kwanza la kutupeleka kwenye kujitegemea litakuwa ni maendeleo ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo Blueprint ambayo ipo tayari, ilitengenezwa tangu mwaka 2018. Hii ingetusaidia sana katika uwekezaji kwenye sekta mbalimbali. Inazungumzia hasa taratibu za kuwezesha kuharakisha uwekezaji ili kufikia Tanzania ya Viwanda. Hata hivyo, ukiangalia utaona tunasuasua na ninyi ni mashahidi. Hata wale wawezeshaji waliokuja Jumamosi wakatupa semina walisema kwenye viwanda tunakwenda katika pace ndogo sana. Sasa naomba tujiulize, tumekwama wapi? Nami naomba tu sasa tuombe Mungu wetu atusaidie ili tutoke hapo na kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ina viwanda 35 vya korosho vyenye capacity ya kubangua tani 50,000 kwa mwaka. Pamoja na kupewa fursa ya kununua malighafi katika minada ile ya awali, wenye viwanda hivi wamekuwa wakibangua chini ya asilimia 10 tu ya korosho yote ambayo inazalishwa katika nchi yetu. Tuseme kwa mfano kama mwaka 2020 korosho iliyozalishwa ilikuwa zaidi ya tani 200,000, ilikuwa ni tani kama 210,000 hivi, lakini ubanguaji haukufikia hata tani 20,000. Kwa hiyo, hii ni below 10%. (Makofi)

Mheshimwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia tena utaona kwamba kuna baadhi ya wenye viwanda walinunua korosho ghafi na wakaiuza nje korosho ghafi badala ya kupeleka kubangua; na kuna baadhi ya viwanda havikubangua hata kilo moja ya korosho. Sasa nashauri tu tuongeze viwanda vya korosho hapa nchini viende sambamba na ongezeko la uzalishaji; tusiache ikawa ongezeko la uzalishaji wa korosho ni kwa ajili tu ya kusafirisha nje. Hata hivyo, tuondoe vikwazo ambavyo vipo katika ubanguaji wa korosho na kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna gesi asilia. Sasa sina hakika kama kweli haina sulphur hii gesi asilia. Nashauri kama kweli kuna sulphur ya kutosha, basi tuitumie hii viwandani ili iweze kuzalisha sulphur kwa ajili ya mbolea na viuatilifu. Kwa sababu mwaka huu tumenunua sulphur ambayo ni takribani shilingi bilioni 25,000/= na kila mwaka tunanunua sulphur kutoka nje. Kwa hiyo, inaweza ikatusaidia, tukianzisha viwanda vitatumia hii sulphur kutokana na gesi asilia tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo fursa nyingi sana. Kwa mfano, mikoa hii ya Dodoma na Singida tuna ubuyu ambao uko porini. Hatuupalilii, hatupulizi dawa; tuna ukwaju, hatuupalii, hatupulizi dawa; lakini tunaona wenzetu wa Uarabuni wanatutumia hapa tende zimekuwa packed vizuri sana. Niseme tu, ubuyu una matumizi mengi zaidi ya 300 na kikubwa katika afya. Una vitamini C nyingi sana. Tunapoenda hospitali wagonjwa wa Corona tunapewa Vitamic C tunamung’unya, lakini hata ukimung’unya ubuyu, gram 20 ambayo ni vijiko viwili tu vya unga wa ubuyu, tayari ni zaidi ya 58% ya daily recommended allowance ya vitamin C. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekti, ubuyu na ukwaju unasaidia sana kukinga magonjwa ya kansa, inasaidia sana pia kupunguza risk za maradhi ya moyo na matunda haya pia yanasaidia kuimarisha mifupa. Hata kwa wazee ni matunda mazuri sana. Kwa hiyo, kimsingi tufanye tu value addition, tuweke viwanda vya kusindika ubuyu na ukwaju kwa sababu kazi yake wala siyo ngumu kiasi kile, ni sawasawa na wanavyofanya wenzetu katika tende.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kidogo.

MWENYEKITI: Malizia.

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri tu sasa kwamba tulinde mapori yetu tusichome moto ovyo, tusikate miti ili kusudi huu ubuyu na ukwaju uendelee kutusaidia. Pia hata watafiti waangalie namna gani ambavyo tunaweza tukaitunza katika kufanya uzalishaji wa kitaalam tuweze kuendelea kuyapata. Kwa kifupi kabla sijamaliza, niseme tu, tukianzisha viwanda vingi tutaongeza ajira na hasa kwa akina mama na vijana ambazo zitatupunguzia umasikini wa mtu mmoja mmoja lakini pia zitaongeza pato la Taifa kwa sababu viwanda vitalipa kodi ya mapato na VAT. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na nimeshamaliza. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuniwezesha kusimama na kuzungumza mbele ya Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuchukuwa nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa ushindi wa kishindo alioupata katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2015. Vilevile namshukuru kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na imani yake kwangu, naahidi kutekeleza majukumu yangu kwa weledi na juhudi kubwa ili kumsaidia Mheshimiwa Waziri katika kutekeleza majukumu aliyopewa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nampongeza Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kuchaguliwa tena kuiongoza Zanzibar katika kipindi kingine cha miaka mitano. Natumia fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kuwa Makamu wa Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kuteuliwa na Rais kuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vilevile nawapongeza Mawaziri wote walioteuliwa kuongoza Wizara mbalimbali katika Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa napenda kumpongeza Spika, Mheshimiwa Job Ndugai; Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson Mwansasu, wewe mwenyewe pamoja na Wenyeviti wote kwa kuchaguliwa kuliongoza Bunge la Kumi na Moja la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumshukuru sana Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Nape Moses Nnauye, kwa kunielekeza na kuniongoza katika kufanya maamuzi sahihi yanayohusu utekelezaji wa shughuli zinazohusu sekta ya habari, utamaduni, sanaa na michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee kabisa, nawashukuru wanawake wa UWT Mkoa wa Mtwara kwa kunichagua kwa kipindi cha tatu kuwa Mbunge wao kupitia tiketi ya Viti Maalum. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sitakuwa nimetenda haki pasipo kuishukuru familia yangu, hasa mume wangu mpenzi, Bwana Laurent Werema Paul na watoto wangu kwa ushirikiano wao mkubwa wanaonipa na kunitia moyo katika kutekeleza majukumu yangu ya kazi za kila siku za Wizara ninazozifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, timu ya Yanga katika historia ya nchi yetu imeweka rekodi kwa mara nyingine baada ya rekodi ya mwisho iliyowekwa na timu ya Simba mwaka 2003. Napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza sana timu ya Yanga kwa kuwa Bingwa wa Soka Tanzania Bara, lakini pili kushiriki Kombe la Washindi Bara la Afrika; na ni matarajio yetu kwamba wataingia hatua ya makundi baada ya mechi yao na timu ya Angola na hasa kutokana na ushindi walioupata katika mechi ya kwanza katika Uwanja wa Taifa Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja ya Wizara yetu na baada ya kusema hayo, naomba sasa kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya kwanza ambayo inahusu kutokuwepo viwanja vya michezo katika ngazi za Mkoa, Halmashauri na shule. Hoja hii imetoka kwa Waheshimiwa wafuatao; Mheshimiwa Kasuku Bilago, Mheshimiwa Lucy Owenya, Mheshimiwa Stanslaus na Waheshimiwa Wabunge wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kila Halmashauri, nadhani tunatambua kabisa kwamba kuna Kamati za Mipango Miji na vilevile kuna Baraza la Madiwani na Wabunge sisi ni miongoni mwa Baraza la Madiwani. Sasa Wizara tunasisitiza kabisa kwamba Halmashauri kupitia Baraza la Madiwani na Kamati ya Mipango Miji watenge maeneo katika kila shule. Watakapokuwa wanatenga maeneo ya shule tunawaomba Halmashauri wakumbuke kuacha maeneo ya kutosha kwa ajili ya viwanja vya michezo ili hata watakapokuwa wakiongeza majengo, lazima yabaki maeneo kwa ajili ya michezo. Vilevile katika ramani za makazi, tunaomba Halmashauri wahakikishe kwamba wanaacha viwanja vya michezo katika makazi ili wananchi waweze kufanya mazoezi na kucheza michezo mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawaomba Waheshimiwa Wabunge wasimamie zoezi hili na wahakikishe kwamba wanafanya ukaguzi katika maeneo ambayo yametengwa ili kuona kama viwanja vya michezo vipo. Kuhusu ubora, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) litakuwa likikagua ili kuangalia ubora wa viwanja hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya pili ambayo inahusiana na kutokuwepo watumishi wa sekta ya habari, utamaduni, sanaa na michezo katika baadhi ya Halmashauri. Waliochangia wameonyesha kwamba pia hata zile Halmashauri ambazo zina watumishi hawa, bado kuna matatizo kwamba wanakosa vitendea kazi. Sasa sisi kama Wizara tumeshaongea na Wizara ya TAMISEMI ili ianzishwe Idara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika kila Halmashauri. Hii tunaamini kabisa itasaidia Idara hii kuwa na fungu lao la bajeti ili waweze kuwa wanapata vitendea kazi na kuwawezesha kufanya shughuli zao kwa ufanisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo kubwa ni kuendeleza sekta hizi za habari, utamaduni na michezo kuanzia ngazi za chini na tunataka Wizara iwafikie wananchi vijijini kupitia Idara hii. Lengo lingine ni kwamba tunataka Wizara iwe na mfumo mzuri wa upatikanaji wa taarifa kupitia Idara hii ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ili tuweze kupanga vizuri shughuli za maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja nyingine ya tatu ambayo imetolewa na Mheshimiwa Martha Mlata na Wabunge wengine, ni kutaka wasanii wapatiwe ardhi lakini vilevile kuwepo kituo kwa ajili ya sanaa za aina mbalimbali. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba Wizara tumeshaongea na Wizara ya Ardhi kwa ajili ya suala hili na upatikanaji wa ardhi utakuwepo kwa sababu Wizara ya Ardhi imeshaanza kulishughulikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Kituo cha Sanaa na Utamaduni, Wizara tayari tumeshapata eneo la ekari 25 katika eneo la Kiromo, kule Bagamoyo na taratibu za ujenzi zitafuata, lakini vilevile kwa wale watu binafsi ambao wanapenda kuingia, sekta binafsi ambazo zitapenda kuingia ubia ili kuweza kuharakisha ujenzi tunawakaribisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya nne ambayo imegusiwa pia na wachangiaji wengi, ni kutokuwepo usikivu wa redio ya TBC katika baadhi ya Wilaya za nchi yetu.
Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba Wizara tayari imeshatenga fedha za maendeleo katika bajeti ya mwaka huu 2016/2017 kwa ajili ya Mkoa wa Kigoma ambayo itaongeza usikivu katika Wilaya za Kasulu na Kakonko, Mkoa wa Mara Wilaya ya Tarime, usikivu katika Mkoa wa Ruvuma Wilaya ya Nyasa, Mkoa wa Tanga Wilaya ya Mkinga, Mkoa wa Arusha Wilaya za Longido na Ngorongoro, Mkoa wa Kilimanajro Wilaya ya Rombo na Mkoa wa kipindi hiki cha mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge wakubali kupitisha bajeti yetu ili tuweze kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutupa fursa hii ya kuweza kujadili masuala yanayohusu maendeleo ya nchi yetu kwa muktadha wa uendelezaji wa Sekta za Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Watanzania wenzangu wote kutoa pole kwa msiba huu uliotupata na Mungu atupe faraja kama wazazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kumpongeza sana Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kusimamia vizuri Serikali na hasa kwa upande wa mapato na matumizi hadi kupelekea Wizara yetu kuongezewa bajeti kwa asilimia 19 kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Pia nimpongeze Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti kwa kuliongoza Bunge kwa weledi, lakini pia Waheshimiwa Wabunge wote kwa umoja na ushirikiano walionao katika kuwatetea wananchi na kuboresha bajeti ya Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii ya kipekee kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe, Waziri wangu, kwa hotuba nzuri ya Bajeti ya Wizara aliyoitoa tarehe 5 Mei, 2017 ambayo utekelezaji wake utaleta matokeo na mageuzi makubwa katika kuimarisha sekta za habari, utamaduni, sanaa na michezo nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri wangu kwa ukarimu wake mkubwa kwangu, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Wakuu wa Idara na Taasisi pamoja na watumishi wa Wizara yangu kwa ushirikiano wanaonipa katika kazi zangu za Naibu Waziri. Niwashukuru wanawake wote wa UWT wa Mkoa wa Mtwara kwa kuendelea kushirikiana na mimi na kuniombea pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee nasema ahsante kwa familia yangu inayoongozwa na mume wangu mpenzi Laurent Werema, kwa kunivumilia, kunitia moyo na kuniombea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii, naomba na mimi nichangie kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianzie na sekta ya habari. Katika sekta hii tuna kundi la kwanza ambalo ni TBC ambapo Kamati iliitaka Serikali kulipa shirika uwezo wa kujiendesha. Wizara na TBC tayari zimelifanyia kazi suala la tozo ya visimbuzi (ving’amuzi) na andiko kuhusu tozo hii mpya linafanyiwa kazi na Wizara ya Fedha na liko katika hatua nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine la Kamati ni kwamba TBC ijenge studio ya kisasa Makao Makuu Dodoma. Fedha za kuboresha studio za TBC Dodoma zimetengwa katika bajeti ya mwaka 2017/2018. Tukiangalia ukurasa wa 79 katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri fedha hizi zinaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pamoja na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wameitaka Serikali kuimarisha usikivu wa TBC na utendaji, lakini pia kuboresha maslahi ya wafanyakazi. Ni kweli kwamba TBC inakabiliwa na changamoto ya uchakavu wa mitambo lakini hata hivyo Serikali imeanza kuchukua hatua zifuatazo katika kutatua kwa awamu changamoto za shirika. Katika mwaka ujao wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga fedha za matumizi ya kawaida na bajeti ya maendeleo kutoka shilingi za Kitanzania bilioni moja hadi shilingi bilioni tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi bilioni moja kwa mwaka 2016/2017 imeshapatikana na hii ni kwa ajili ya kuboresha usikivu katika maeneo matano ya mipakani na moja ni Kakonko (Kibondo), Mheshimiwa Kasuku kama yupo amelipigia sana kelele suala hili kwa hiyo awaambie watu wake wakae mkao wa kula. Pia katika Wilaya za Nyasa, Longido, Rombo, Tarime na leo pia nimesikia Mheshimiwa Ngonyani akilipigia kelele, kwa hiyo, wananchi wa Nyasa nao wakae tayari kwa ajili ya usikivu wa TBC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Kamati pia ambalo linaitaka Wizara ihamishe mashine ya zamani ya TSN ya kuchapia magazeti ifungwe Dodoma ili kurahisisha upatikanaji wa magazeti. Wizara itafunga mtambo mpya Dodoma na hii ni kwa sababu kitaalam mtambo wa zamani ukifunguliwa na kuhamishiwa Dodoma unaweza kuharibika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya utamaduni; Kambi Rasmi ya Upinzani iliitaka Serikali kukuza utalii wa kiutamaduni na majibu yake ni kwamba Serikali imeendelea kuratibu, kusimamia na kutangaza bidhaa za utamaduni na kufanya maonesho na matamasha ya fani mbalimbali za utamaduni ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kuvutia utalii na kuingiza mapato.

Mheshimiwa Spika, kuna mchangiaji mmoja pia alipendekeza kwamba kila mkoa kuwe na makumbusho lakini hili ni suala la Wizara ya Maliasili na Utalii chini ya Kitengo cha Malikale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kudhibiti mmomonyoko wa maadili ambalo limechangiwa na Wabunge kadhaa. Maadili ni mwenendo unaokubalika na wengi katika utendaji kazi au uendeshaji wa maisha. Kwa hiyo, suala hili ni la watu wote na inatakiwa lianzie katika familia hadi katika taasisi. Hata hivyo, Wizara inaendelea kutoa elimu kuhusu uzingatiaji wa maadili ya Mtanzania na kuchukua hatua mbalimbali za kisheria pale panapotokea ukiukwaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maendeleo ya sekta ya sanaa, Kamati imeitaka Wizara iendelee kupambana na wizi wa kazi za wasanii. Wizara inaishukuru Kamati kwa kuunga mkono jitihada za Wizara na pia kwa kutoa msimamo wake kwa kuwataka wote wanaohusika na uharamia wa kazi hizo kuacha mara moja. Aidha, Wizara inakubaliana na ushauri wa Kamati kuhusu uboreshaji wa kazi hizo na itaendelea kushirikiana na wadau kuwajengea uwezo ili kuboresha kazi zao ili waweze kuendana na maendeleo ya teknolojia na kushindana katika soko la ndani na la nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Kamati imehimiza uboreshaji wa filamu za ndani na wananchi pia kununua kazi za ndani. Ushauri huo wa Kamati umepokelewa na utafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Kambi ya Upinzani katika sekta ya sanaa kwamba matumizi ya stempu za TRA kutofanya kazi vizuri kutokana na teknolojia ya mtandao. Stempu hizo hutumika kubandikwa katika DVD na CD ambazo kwa sasa ndiyo mfumo unaotumika kusambaza kazi hizi hapa nchini. Kutokana na ukuaji wa teknolojia tayari taratibu za kutengeneza stempu katika nakala laini zinaendelea na stempu hizi toka zimeanza kutumika zimefanikisha kubaini na kukamata kazi zisizo halali zenye thamani ya shilingi bilioni 5.1.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi Rasmi ya Upinzani pia ilionesha kwamba kuzuia kazi za nje ya nchi sio kinga ya wizi wa kazi za filamu na muziki. Serikali haijazuia filamu za nje bali inazitaka kufuata sheria, kanuni na taratibu. Kwa hiyo, dhana hii kwamba tunazuia kazi za nje si kweli, tunataka utaratibu ufuatwe na sheria vilevile zizingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya Wizara ni kulinda mila na desturi zetu na kulinda kazi za wasanii na hatutakubali ukiukwaji wa utamaduni wetu na hatutakubali pia kazi za nje ziingie katika nchi yetu bila kufuata utaratibu. Wizara yangu iliwasilisha barua TAMISEMI kuwaomba wawasiliane na mikoa yote ili kuona namna bora ya kuondokana na filamu zisizofuata utaratibu. Kwa hiyo, utekelezaji wa maelekezo ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ni kwa nchi nzima. Kwa hiyo, tusichukulie kwamba kwa kuwa yeye ametekeleza kwamba ni uamuzi wake.

Mheshimiwa Spika, nimeshasema kwamba Wizara iliandika barua TAMISEMI na kuomba wawasiliane na mikoa yote ili kuona namna bora ya kuondokana na filamu zisizofuata utaratibu, kwa hiyo, mikoa yote inatakiwa kufuata na kuzingatia agizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la upatikanaji wa Vazi la Taifa ambalo nalo limechangiwa na Wabunge kadhaa. Suala hili lilifikia katika ngazi ya Baraza la Mawaziri na uamuzi ulikuwa kwamba Vazi la Taifa litokane na kuamuliwa na wananchi wenyewe. Nikitoa mifano tu ni kwamba hata kipindi cha zamani ilikuwa inatokea mama zetu tulikuwa tukiwasikia wanasema leo tuvae Kitaifa, lakini hapa katikati pia lilizuka vazi fulani ambalo linatokana na kitambaa cha kitenge (makenzi) likaenda mpaka kutaka kuwa kama Vazi la Taifa. Kwa hiyo, ni vyema wananchi wakaamua sasa tuvae vazi gani kama ndiyo Vazi la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kuboresha soko la ndani la tasnia ya filamu na kusimamia mapato ambapo tayari wapo watayarishaji wa filamu ambao wameendelea kutengeneza filamu nzuri zilizoweza kuingia kwenye soko la ushindani la ndani na nje ya nchi. Hata hivyo, hoja ya uwepo wa filamu za nje zisizofuata taratibu zimefanya soko la ndani kukumbwa na ushindani mkubwa na Serikali na wadau husika kukosa mapato. Serikali katika kuboresha soko la ndani imeendelea kuwajengea uwezo watayarishaji na wazalishaji wa filamu ili kufanya kazi zao kwa weledi na kwa ubora wa hali ya juu kama inavyoelekezwa kwa kina katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 32.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la uboreshaji wa tasnia ya ulimwende ambalo limechangiwa na wachangiaji kama wawili hivi. Tasnia ya ulimwende imeendelea kuendeshwa nchini kutoka mwaka 1994 na imeendelea kuwa na mafanikio makubwa hasa katika kuitangaza nchi na vivutio vyake ndani na nje ya mipaka ya Tanzania. Baadhi ya maeneo yaliyofanyiwa kazi ni pamoja na waandaaji kurekebisha dosari mbalimbali zilizojitokeza na kuwa na mfumo bora na uwazi wa uendeshaji wa mashindano mbalimbali ya ulimwende.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Miss Tanzania, Wizara katika kulinda hadhi ya shindano hilo imetoa maagizo yafuatayo kwa waandaaji wa shindano hilo (Lino International Agency). Lino International Agency ihakikishe kwamba Kamati ya Miss Tanzania inatoa zawadi ya gari kwa mshindi wa Miss Tanzania 2016 na washiriki wengine wote wanaodai zawadi zao ndani ya mwaka huu kabla ya Juni, 2017 na endapo wakikaidi ama wakishindwa kutoa zawadi katika muda huo watakuwa wamejitoa wenyewe kwenye biashara hii na sheria itachukua mkondo wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kuitaka Serikali ikamilishe utungwaji wa Sera ya Filamu. Tayari maandalizi ya Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Filamu yamefikia hatua ya kupata rasimu ya sera. Wadau mbalimbali wametoa maoni na rasimu hiyo itawasilishwa katika ngazi za maamuzi mwishoni mwa mwezi Juni, 2017. Rasimu hiyo ya sera imezingatia pamoja na mambo mengine umuhimu wa kuanzishwa kwa shule ya filamu (film school).

Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo ya michezo. Katika sekta ya maendeleo ya michezo kuna hoja iliyojitokeza ya CCM kurejesha viwanja vyake Serikalini. Hili suala limetolewa ufafanuzi mara kadhaa hapa Bungeni lakini hata hivyo niendelee kusema tu tena kwamba viwanja hivi ni vya CCM kwa sababu hatimiliki ni ya CCM. Niseme tu tena kwamba haipo hati ambayo inaonesha kwamba kuna kiwanja kilikuwa cha mmiliki mmoja kikahamishiwa kwa CCM, kwa hiyo tuelewe wazi kwamba hivi viwanja ni vya CCM. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameitaka Serikali ijenge na kulinda viwanja na maeneo ya wazi. Kwa mujibu wa Sera ya Maendeleo ya Michezo ya Mwaka 1995 inaelekeza kuwa jukumu la ujenzi wa viwanja linashirikisha wadau wote ikiwemo Serikali na wadau wengine. Serikali katika juhudi zake za kuboresha miundombinu ya michezo inashirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje kujenga miundombinu kwa ajili ya matumizi ya michezo.

Mheshimiwa Spika, katika kufanikisha azma hiyo, Serikali imejenga Viwanja vya Taifa na Uhuru na sasa inajiandaa kujenga Uwanja wa Dodoma. Aidha, mamlaka mbalimbali na wadau nchini wanahamasishwa kushiriki kama walivyoanza baadhi kama vile Azam, Halmashauri ya Bukoba Mjini, Liwale, Lindi na kadhalika na taasisi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa wito kwa wadau mbalimbali wa michezo wakiwemo Waheshimiwa Wabunge kuhakikisha kuwa halmashauri zao zinatenga maeneo na bajeti kwa ajili ya ujenzi wa viwanja vya michezo. Aidha, natoa wito kwa mamlaka zinazohusika kuhakikisha kuwa viwanja vyote vilivyovamiwa katika maeneo yao vinarejeshwa ili viweze kutumika kwa shughuli za michezo na burudani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba yupo mdau mmoja muhimu sana katika kuendeleza viwanja vya michezo ambaye ni TFF. Kwa taarifa ni kwamba kwa sasa ule Uwanja wa Tanga uko mbioni kuanza kujengwa mwaka huu, wanasubiri tu bajeti ipitishwe ili waweze kuujenga. Vilevile kama nilivyosema hapo awali, viwanja vya Lindi na Memorial Moshi viko kwenye list ya ukarabati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niseme tena naunga mkono hoja, ahsanteni.
Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hoja yetu hii ya Azimio la Mkataba wa Kudhibiti Matumizi ya Dawa na Mbinu Haramu katika Michezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kukupongeza kwa kazi nzuri ambayo unaifanya, kwa kuliendesha Bunge kwa kutumia Kanuni vizuri. Vilevile niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia katika hoja yetu hii na nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa jinsi alivyowasilisha hoja kwa umahiri mkubwa. Hongera sana Mheshimiwa Waziri wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na faida kubwa ambazo ziko katika mkataba huu tunaona hakuna vipengele vyovyote ambavyo hatuhitaji kuviridhia, kwamba hakuna reservations. Kwa hiyo ni mkataba mzuri, hii inaonesha wazi kabisa huu ni mkataba mzuri na ndiyo maana hakuna reservations zozote.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianzie tu na hili la kijana wetu huyu aliyepatwa na dalili, hakukutwa moja kwa moja na madawa lakini kulikuwepo na dalili ambazo zinaashiria kwamba kulikuwa na dawa za kuongeza nguvu kule Brazil, akafungiwa kwa miaka miwili. Sasa kutokana na hilo inaonekana kwamba mwaka 2015/2016 zimechukuliwa sample 14 na kupelekwa katika Maabara za Kimataifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bahati nzuri tunashukuru sana Wizara inafurahi na ina faraja kwamba sampuli zote hizi 14 hakuna hata moja ambayo ilikutwa na dalili za kuwepo na matumizi ya dawa au mbinu za kuongeza nguvu michezoni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mkataba huu una manufaa makubwa, mojawapo ni lile la kutoa elimu pamoja na mafunzo kwa vijana wanamichezo wetu pamoja na watalaam wengine, lakini pia inatoa fursa kubwa sana za utafiti. Nami nichukue fursa hii sasa kutoa wito kuwaomba watafiti wetu wajiandae, pale ambapo mkataba huu utakapokuwa umeanza kufanyakazi kuna maeneo mengi sana ya kufanyia utafiti na yanaelezwa katika vifungu mbalimbali vya mkataba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, wanaweza wakafanya utafiti katika maeneo ya saikolojia, maeneo ya utu wa wanamichezo, physiology, wanaweza wakafanya pia utafiti katika sayansi ya michezo, wanaweza pia wakafanya utafiti katika vitu mbalimbali ambavyo vinajitokeza kulingana na maendeleo ya kiteknolojia, kuna vitu vipya ambavyo vinaweza vikajitokeza kama matumizi au dawa za kuongeza nguvu. Kwa hiyo watafiti wetu wajiandae kufanya kazi katika maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja moja ambayo imejitokeza kutoka kwa Mheshimiwa Hafidh Ali alipokuwa akichangia kwamba ni vizuri sasa tukafanya maandalizi. Nafurahi kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba Wizara imeshaanza kufanya maandalizi machache. Kwa mfano, kuna wataalam ambao tayari wameshaanza kupewa elimu ya awali.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tumeshaandaa eneo pale katika uwanja wa Taifa kwa ajili ya ofisi ya National Anti-doping Agency. Kwa hiyo, maandalizi kama hayo yamefanyika. Pia yanatakiwa maandalizi ya kisera, kisheria na kanuni ambavyo napenda kulitaarifu Bunge lako kwamba Wizara yetu imejipanga vizuri kabisa kwa ajili ya hili, kuandaa, kurekebisha sera na kufanya marekebisho, kuipitia upya pia sheria yetu ya michezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Hafidh Ali pia katika mchango wake aligusia jambo ambalo naona pia ni muhimu sasa watafiti tutawaomba wajiandae kulifanyia kazi, kwamba kuna watu ambao unaona kabisa umri umepita lakini wanacheza vizuri tu mpira na amekuwa na mashaka kwamba labda kuna vitu wanavyotumia. Kwa hiyo, hili ni eneo ambalo pia watafiti wanaweza wakalifanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja nyingine ambayo inahusiana na matumizi ya bangi na pombe katika michezo. Suala la pombe lipo limezuiliwa na liko katika kundi la alcohol, lakini kuzuiwa kwake ni wakati wa mashindano tu. Kwa hiyo hili nalo tutaliangalia, wakati wa kutunga sheria nitaomba Bunge lako pia liangalie kama kweli izuiliwe kwa wanamichezo wakati wa mashindano tu au sasa watazuiwa moja kwa moja sijui, lakini bangi inazuiwa na iko katika kundi la cannabinoids. Bangi inazuiwa kabisa, hairuhusiwi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja nyingine ambayo ameichangia Dkt. Ndugulile kwamba, hata zile dawa ambazo ni za tiba zinazuiliwa. Naomba kumtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, kipo Kifungu cha 34 katika Mkataba huu na hiki Kifungu kinaruhusu sasa ile World Anti-Doping Agency, kufanya Amendments kwa ile list ambayo ni prohibited list ili therapeutic use exemptions. Kwa hiyo utaona kwamba, hii WADA ikifanya amendments masuala ya dawa kwa ajili ya matumizi ya kiafya yanaweza yakaruhusiwa kutumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru tena kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja. Ahsante sana!
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hongera sana Mheshimiwa Waziri, Dkt. Philip Mpango na Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji kwa kazi nzuri mnayolifanyia Taifa letu. Kazi kubwa ni pamoja na ongezeko la ukusanyaji wa mapato ambayo yamepelekea kulipa deni la Taifa kwa kiasi kikubwa. Nina ushauri katika eneo la misamaha ya kodi inayotolewa katika sekta mbalimbali kama vile kilimo, mifugo, afya, michezo, elimu na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ingekuwa vema wataalam wakaisaidia Wizara kutaja vitu vyote vionekane katika sheria ili kuondoa usumbufu kwa maafisa wa TRA wanaohusika na utozaji kodi, kwani inapotokea jina la kitu husika hakikutajwa katika sheria wanalazimisha kutoza kodi. Vilevile sera ya michezo inaelekeza kutoa unafuu wa kodi kwa vifaa vya michezo na kutotoza kodi kwa vile vifaa ambavyo vimetolewa kama msaada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili kuna malalamiko mengi kutoka kwa wananchi ambao ni wadau wa michezo kwamba vifaa vya michezo vilivyotolewa kama msaada vinaozea bandarini. Hata hivyo, Mheshimiwa Makamu wa Rais aliahidi suala hili kufanyiwa kazi siku alipokuwa akizindua mazoezi ya viungo ya kila Jumamosi ya pili ya kila mwezi mwaka jana Novemba, 2016. Naomba Wizara ilifanyie kazi suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naitakia Wizara kila kheri na naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Maghembe na Naibu wake Engineer Ramo pamoja na timu nzima ya Wizara kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika Wizara ya Maliasili.

Mheshimiwa Mwenyekiti mchango wangu uko katika maeneo mawili, kwanza ni kuhusu utalii wa utamaduni, lakini pili nimalizie kuhusu suala la Vazi la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukiri kabisa kwamba tuna vivutio vingi vya utalii wa utamaduni katika nchi yetu kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge wenzangu, lakini Wizara yetu ina kazi kubwa, iko katika mchakato wa kutekeleza Mkataba wa UNESCO wa mwaka 2003 ambao unahusu Urithi wa Utamaduni Usioshikika na ule mkataba wa mwaka 2005 wa Kulindwa na Kukuzwa kwa Uanuai wa Kujieleza Kiutamaduni.

Sasa tunachofanya sisi Wizara ni kukusanya taarifa na tafiti kutoka kwa wadau mbalimbali zikiwemo Halmashauri, na taarifa hizi zinahusu maeneo ya kihistoria, kimila, kidesturi na vivutio vya utalii wa kiutamaduni.

Mheshimiwa Mwenyekiti katika zoezi hili tunashirikiana kwa karibu kabisa na Wizara ya Maliasili, Kitengo cha Malikale pamoja na TAMISEMI na zoezi hili ni endelevu na uendelevu wake utaona kwamba kuanzia mwezi Agosti, 2016 hadi sasa tumeshapata vivutio vipya kutoka Halmashauri 35 na Mikoa 19. Lengo kumbwa ni kuzitumia taarifa hizi katika kuwasaidia wananchi kuweza kutumia utalii wa kiutamaduni kuongeza kipato. Kwa hiyo, nitoe wito kwamba Halmashauri zote ziendelee na zoezi hili na tuna dhamira kubwa ya kutumia baadhi ya mila na desturi zetu katika kuzipeleka kwenye orodha wa Urithi wa Utamaduni wa Dunia. Kwa mfano, mila na desturi ya jando na unyago ambayo iko katika Mikoa ya Kusini na Mikoa ya Ukanda wa Pwani kama vile Wamakonde; na ile mila ya Wamasai ya kurithisha ngazi ya rika ya kipengele cha Engpaata Yunoto na Olng’esher. Kwa hiyo, vivutio hivi vikiingia katika Orodha ya Urithi wa Dunia vitasaidia sana kuwa vivutio vya utalii wa utamaduni katika yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi binafsi nikiri kwamba nimeshawahi kutembelea baadhi ya vivutio na niseme tu kwamba bado Halmashauri zetu zina kazi kubwa ya kuhakikisha kwamba zinaboresha mazingira katika maeneo yale ya vivutio. Kwa mfano, Halmshauri hizi zihakikishe kwamba kunakuwepo na vyoo, barabara nzuri, maeneo ya kulia chakula kwa sababu vivutio vingine vingi viko katika maeno ya maporini, lakini ni vizuri sana. Kwa mfano nilishawahi kufika katika kichuguu ambacho kinacheza kule Babati, kunahitajika maboresho ili kusudi watalii wengi waweze kufika. Nishauri tu Halmashauri zione umuhimu wa kutenga bajeti ili kusudi kuweza kuboresha maeneo hayo Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa upande mwingine nizishauri halmashauri pia ziwatumie wacheza filamu pamoja na waigizaji katika maeneo yao kwa kuwapa mikopo ili kusudi waweze kucheza filamu za…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia kwa maandishi. Napongeza hotuba nzuri ya Wizara ya Maji ikiongozwa na Mheshimiwa Kamwelwe na timu yake. Naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani kwa Mkoa wa Mtwara kutengewa kiasi cha shilingi bilioni 12.9 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji vijijini (mwaka 2018/2019). Katika miradi ya kimkakati Wilaya ya Tandahimba imetengewa shilingi bilioni moja. Kutengewa ni jambo moja na kupewa ni hambo lingine. Nasema hivi kwa sababu mwaka 2017/ 2018 Serikali ilitenga shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya Mradi wa Mkwiti Group Water Supply Scheme ambao utahudumia wananchi zaidi ya 36,000 katika Wilaya ya Tandahimba. Cha kushangaza hakuna fedha ambayo imetolewa hadi sasa. Wilaya ya Tandahimba ina wakazi takribani 243,000 lakini upatikanaji wa maji ni asilimia 24 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maombi, mkandarasi ameshaandaa vifaa viko katika eneo la mradi kwa asilimia 80. Kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa ameomba advance ya shilingi milioni 400 lakini hajapewa hadi sasa. Ameomba shilingi bilioni moja kwani amekidhi certificate, lakini hajapewa. Tafadhali mkandarasi apewe fedha hii ili aweze kufukia mabomba na kukamilisha phase one vinginevyo mabomba yataibiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili Halmashauri inaomba kibali cha kupata shilingi bilioni 8.5 zote ili watekeleze phase zote nne za Mradi wa Mkwiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, Halmashauri ipate kibali cha kuanzisha Mamlaka ya Maji ya Tandahimba.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika bajeti hii muhimu. Kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia neema zote katika maisha yangu. Vilevile nimpongeze sana Waziri Mheshimiwa Mbarawa pamoja na Naibu Mawaziri wake, Makatibu Wakuu pamoja na timu yote ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kazi nzuri ambayo wanafanya katika Wizara hii muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue pia nafasi hii kuipongeza sana Serikali yetu ya Awamu ya Tano, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuvunja rekodi ya bajeti ya Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi kwa sababu imetenga shilingi trilioni 4.2, ni kitu ambacho hakijawahi kutokea, hongera sana Serikali. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa ajili ya kuruhusu kazi ifanyike katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuunga mkono hoja kwa asilimia 100. Naunga mkono hoja ili fedha hii ambayo imetengwa iweze kutoka kazi iende kufanyika katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa Mkoa wetu wa Mtwara katika fedha hizi ambazo zimetengwa imepata zaidi ya shilingi bilioni 42. Nichukue nafasi hii kwa niaba ya wana Mtwara kushukuru sana Serikali kwa sababu fedha hizi zinakwenda kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Mkoa wa Mtwara takribani shilingi bilioni 12.8 na shilingi bilioni 10 kwenye ujenzi wa barabara yetu ya uchumi ya Mtwara – Tandahimba - Newala - Masasi na nyingine zilizobaki zinakwenda kufanya matengenezo ya barabara za mkoa na barabara kuu za lami pamoja na zile za changarawe. Pamoja na hayo pia fedha hii inakwenda kutengeneza madaraja, kutengeneza maeneo korofi na kazi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inatia faraja kwamba fedha hizi siyo kwamba zinakwenda Mtwara tu, kuna fedha kiasi tofauti kinakwenda katika mikoa mingine. Kwa mfano, nichukulie katika utengenezaji wa viwanja vya ndege utaona kuna fedha zinakwenda kutengeneza Kiwanja cha Kigoma, Mpanda, Tabora, Songwe, Mwanza, Arusha, Mtwara ipo pia, Sumbawanga, Shinyanga, Kilimanjaro, Geita, Iringa, Musoma, Songea, Dodoma, Tanga, Manyara, Lindi, Simiyu, ni maeneo mengi tu fedha inakwenda kutengeneza viwanja vyetu vya ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, naomba ninukuu maneno ya wanafalsafa ambao wanasema kwamba, everything will be okay in the end. If it’s not okay, it’s not the end. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Mbarawa asonge mbele, kwa sababu huu siyo mwisho wa kazi mwaka ujao naamini kabisa wataendelea katika maeneo mengine.

Pamoja na hayo niombe kutoa kilio cha wana Mtwara katika eneo la barabara ya Mtwara – Tandahimba - Newala - Masasi. Mwaka uliopita tuliambiwa kwamba kiasi ambacho kimetengenezwa pale ni asilimia 16 ya kilometa 50 ambalo ni eneo la Mtwara Mnivata. Sasa asilimia 16 ukiangalia itakuwa ni kama kilometa 8 lakini mwaka huu tuna shilingi bilioni 10 za matengenezo ya kipande hicho hicho. Kwa hiyo, ukichukua zile kilometa 200 kuna maeneo mengine tunaambiwa ni kilometa 209 lakini document zingine tunaambiwa ni 221 ni kwamba tunaweza tukachukua miaka mingi sana kumaliza eneo hili. Kwa hiyo, niombe mwaka ujao Wizara iangalie uwezekano wa kuongeza kasi ya matengenezo ya barabara hii kwa sababu ni muhimu sana katika uchumi wa nchi yetu lakini kwa wakulima wa Mtwara kwa sababu mara nyingi unapopita…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwa maandishi. Kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mwijage na Naibu Waziri wake Mheshimiwa Manyanya, pamoja na timu yao ya watendaji wa Wizara kwa jinsi wanavyosimamia vizuri Wizara ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri, ili viwanda vyetu viweze kufanya kazi kwa tija ni lazima kuhakikisha ipo malighafi ya kutosha. Katika mikoa inayolima korosho, msimu huwa unaisha mwezi Desemba, inashangaza sana kuona kwamba wateja wa korosho iliyobanguliwa wanapoagiza bidhaa hii tena tani 50 tu kwa mwezi. Inakosekana kwa madai kwamba hakuna malighafi wakati ambapo mahitaji yenyewe yametoka mwezi wa pili. Hii inamaanisha kwamba uzalishaji katika viwanda vyetu huwa ni kwa kipindi cha miezi mitatu tu (Novemba, Desemba na Januari).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba jitihada ifanyike kufuatilia tatizo ni nini. Je, ni ukosefu wa mitaji ya kununua malighafi ya kutosha au ni kukosa mgao wa kutosha ikiwa na maana ya kibali cha ununuzi kimewabana wenye viwanda? Kaeni na wenye viwanda vya korosho na Wizara ya Kilimo ili kujadili namna bora ya kuwezesha upatikanaji wa korosho kwa viwanda vyetu katika kipindi cha mwaka mzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vyetu vidogo bado vina changamoto kubwa ya kukatikakatika umeme hovyo na ukosefu wa maji na hivyo kuathiri uzalishaji kwa ufanisi na tija. Wizara ya Viwanda ikae na Wizara ya Maji na Wizara ya Nishati ili kutafuta ufumbuzi wa tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu itolewe kwa wajasiriamali kuhusu namna ya kuanzisha viwanda vidogo. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwa maandishi. Kwanza niipongeze kazi nzuri inayofanywa na Waziri, Mheshimiwa Dkt. Tizeba na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Mary Mwanjelwa ya kuiongoza Wizara ya Kilimo kwa umahiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri, Wizara iongeze kasi katika kuhimiza uwezeshaji wa kuzalisha high nutritional value crops kama mboga na matunda kwa ajili ya kuimarisha lishe ya jamii. Viazi lishe vyenye vitamin ‘A’ kwa wingi, mbegu yake inatafutwa na wananchi wengi lakini haipatikani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Wizara iwezeshe uzalishaji wa mbegu za viazi lishe ili iweze kupatikana kwa wingi, wananchi waipande na kutumia viazi hivi ili kuimarisha lishe zao. Inasikitisha na kushangaza kuona mboga mboga kama karoti, nyanya na pilipili hoho zinaingia nchini kutoka nchi jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iielekeze Idara za Mipango Miji katika Halmashauri zetu ili Halmashauri ziweze kutenga maeneo ya kutosha katika miji na vijiji kwa ajili ya urban farming ili wakulima na hasa vikundi vya vijana, waweze kulima mboga na matunda ambayo yatawezesha upatikanaji wa malighafi kwa viwanda vidogo mijini na vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maafisa Ugani wahimizwe kwenda kwa wakulima badala ya kubaki ofisini. Wakatoe elimu ya mbinu za kilimo bora, jinsi ya kupambana na visumbufu vya mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia kwa maandishi. Hongera sana Mheshimiwa Waziri Mwigulu na Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Masauni kwa kuliongoza vizuri Jeshi la Polisi, Magereza, Uhamiaji na taasisi zote za Wizara ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri inayofanywa na watumishi wazalendo wa Wizara, lakini wapo wachache ambao wanaharibu taswira ya Wizara. Viongozi wa juu wa Wizara wapite katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu, wasikilizeni kero za wananchi kuhusu utendaji wa baadhi ya Maafisa wa Polisi, Magereza na Uhamiaji ili waweze kuzitafutia ufumbuzi na nyingi zimesemwa humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna moja ambalo limenitokea jana shambani kwangu; Askari walivamia wakampiga mke wa mlinzi ambaye ni mjamzito, wakavunja mlango kwa madai kwamba wanakagua mali ya wizi na hawakukuta chochote. Walitaka kuchukua dawa za mazao ambazo bado hatujazilipia na yule mama akawaambia kwamba watafungwa kwani dawa zina deni, ndipo wakaziacha. Kwa bahati nzuri, mume wangu aliweza kwenda kuripoti kwa mkuu wa kazi wa Askari hao, wakaitwa na kuomba radhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafadhali naomba sana Mawaziri wetu wakemee mmomonyoko wa maadili unaoendelea miongoni mwa Askari wachache kwani jambo baya husambaa na kusikika kwa haraka kuliko jema lililo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza taarifa za kupungua kwa uhalifu ikiwemo makosa ya usalama barabarani. Naamini chanzo kikuu cha mapato kwa Jeshi la Polisi ni faini na kwa uchache stika. Kwa mwaka wa fedha 2017/2018, lengo la kukusanya shilingi bilioni 73 halikutimia na badala yake zimekusanywa shilingi bilioni 43. Sasa kama makosa yamepungua ina maana faini pia zitapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nipate maelezo ya kuridhisha ni kwa nini Wizara kwa mwaka 2018/2019 imeongeza makadirio ya mapato kufikia shilingi bilioni 84? Je, kuna chanzo gani kipya cha mapato? Vinginevyo wananchi watalazimishwa kulipa faini isivyo halali. Leo nitashika shilingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa hongera kwa kazi nzuri Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo, pamoja na Naibu Mawaziri. Pia naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri; Ripoti ya CAG inaonesha hati safi kwa zaidi ya asilimia 90 ya halmashauri zote nchini. Jambo hili lisitufanye kudhani kwamba hata miradi inakwenda vizuri kwa zaidi ya asilimia 90. Hii ni kwa sababu mimi nikiwa Mjumbe wa Kamati ya LAAC nimeshuhudia miradi iliyoripotiwa na Ofisi ya CAG kwamba imekamilika na inatumika sivyo ilivyo, kwani haitumiki kutokana na kutokamilika ipasavyo. Kimsingi miradi yote miwili ya maji tuliyoikagua Mkoani Tabora ilikuwa haitumiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba Wakurugenzi na watendaji wahimizwe na wawezeshwe kutembelea miradi ya maendeleo vijijini na katika maeneo yao ya utawala ili kusimamia miradi kwa ufanisi. Vilevile, Ofisi ya CAG iwezeshwe kwa upande wa rasilimali fedha na rasilimali watu ili waweze kufanya performance audit ambayo itaonesha kama mradi kweli ina tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo inabidi hata Kamati ya LAAC iwezeshwe kufika maeneo mengi zaidi ili kuthibitisha taarifa ya CAG, hivyo, ni vyema ipewe muda wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utafiti uliofanywa na Ofisi ya Waziri Mkuu mwaka 2009 kuhusu umuhimu wa VRTs katika kuhamasisha maendeleo ndani ya mfumo wa Serikali za Mitaa, ilipendekezwa kwamba VRTs wajengewe uwezo waenezwe katika halmashauri zote, wapewe vitendea kazi na usafiri; vilevile uwepo mpango na miongozo sahihi kwa ajili ya kufuatilia utendaji wao. Katika kuhitimisha hoja, ningependa kupata maelezo ni nini kimefanyika kuhusiana na VRTs tangu mapendekezo hayo yametolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti suala la lishe katika halmashauri zetu litiliwe mkazo kwa kuajiri Maafisa Lishe na kusisitiza elimu ya lishe kwa jamii, pia kuhimiza agenda ya lishe katika RCC, DCC na Mabaraza ya Madiwani. Hii itapunguza gharama na bajeti katika Sekta ya Afya.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ya Bajeti ya Serikali. Nianze tu kwa kusema kwamba nami nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya katika Taifa letu; Watanzania wanajua na Mataifa mengi ya dunia hii yanajua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba hata sisi Waheshimiwa Wabunge, tunafanya kazi nyingi katika Majimbo yetu kwa kuhamasisha tu, kwa kuibana Serikali, lakini wakati mwingine kwa kuhamasisha wananchi, zinajengwa Hospitali, zinajengwa shule, lakini barabara pia

zinajengwa na pale wananchi wanatusifia na kutupongeza na kusema Mbunge fulani katujengea barabara, katujengea shule, katujengea hospitali; wakati huo huo pesa hizo zimetoka Serikalini. Sijawahi kusikia Mbunge hata mmoja akikataa wasimpongeze. Nadhani tunakubaliana na hilo. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii pia kumpongeza sana Waziri wa Fedha Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango pamoja Naibu wake, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji kwa kazi Nzuri ambayo wanaifanya katika Wizara yao. Vile vile nawapongeza kwa kutengeneza hotuba nzuri sana ya Bajeti ambayo inagusa maslahi ya Watanzania wote kwa ujumla. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine, kuna baadhi yetu tunasema kwamba Bajeti hii ni hewa kutokana na kwamba tumeweka malengo makubwa na hatukuitekeleza kwa asilimia 100. Namwomba Mheshimiwa Dkt. Mpango, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Naibu wake na timu yote nzima, wakaze buti, tusonge mbele. Kwa sababu wanafalsafa wanasema hivi: “most people fail, not because they aim to high and miss, it is because they aim too low and heat.” Tusonge mbele Mheshimiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono Bajeti hii kwa asilimia mia moja. Ukienda ukurasa 23 hadi wa 25 wa kitabu cha Bajeti utaona mafanikio ya Bajeti ya Serikali ya mwaka 2017/2018 na mafanikio hayo yanatokana na matumizi ya kiasi cha fedha zaidi ya shilingi trilioni nne na zaidi na kati ya hizo, utakuta zaidi ya asilimia 25 yametumika kulipia malimbikizo ya madeni ya watumishi wa Umma, Wakandarasi, pamoja na Wazabuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza sana kwa sababu hili tatizo lilikuwa limeendelea kwa miaka mingi na hii ni ishara nzuri na ni mwanzo mzuri sana kwamba sasa tutakuwa tunapambana na malimbikizo ya madeni. Naomba tuendelee hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe shukrani zangu kwa Serikali kulipa fedha za Mkandarasi ambaye alikuwa anatekeleza Mradi wa Mkwiti Group Water supply Scheme alikuwa akidai advance ya shilingi bilioni 400 lakini amelipwa zaidi ya bilioni 300 na hivyo itamwezesha kuendelea na mradi wa maji katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwamba suala la kutatua tatizo la maji katika Halmashauri ya Tandahimba limepewa kipaumbele na kwa kweli wananchi wa Tandahimba wanashukuru sana, kwa sababu Wilaya hii ya Tandahimba ina watu zaidi ya laki 243 na tatizo la maji ni kwamba upatikanaji wa maji ni asilimia 24 tu katika vijiji, ambacho ni kiasi kidogo sana, iko chini sana na ile average ya Kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Wizara ya Maji ielekeze nguvu zaidi katika eneo hili kwa sababu mwaka jana walikuwa wamepangiwa bajeti bilioni 2.3 na kwa sasa wanaomba Mkandarasi huyu apewe bilioni moja kwa ajili ya certificate ili kusudi aweze kumaliza ile phase one (I).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri pia inaomba wapewe kibali cha kuendelea phase II na phase III ambayo inatarajiwa kutoa huduma kwa takribani wananchi elfu 36 ambao ni asilimia 14, kwa hiyo ukichanganya na zile 24 tutaweza kufikia asilimia 38.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana wadau wa sekta ya maji tusimamie vizuri miradi yetu ya maji kwa sababu Kamati ya LAAC tumetembelea katika maeneo mbalimbali. Katika Halmashauri mbili ambazo tumezitembelea na tulikuwa tumeambiwa kwamba miradi hii imekamika na inatumika, Halmashauri zote mbili miradi haitumiki. Kwa hiyo ni tatizo, tunaweza tukawa tunaitupia Serikali lawama lakini pia Watendaji wanaonesha kutukwamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono na nipongeze sana Serikali kuweka kipaumbele katika sekta ya kilimo. Sekta ya Kilimo ni muhimu, lakini ndani ya sekta ya kilimo kuna suala la lishe na ukiangalia malengo la maendeleo endelevu (SDG), lengo namba mbili ni kipaumbele katika masuala ya lishe. Kwa hiyo, niombe Serikali kupitia Wizara ya Kilimo ishirikiane na taasisi mbalimbali au Sekta mbalimbali sekta ya afya, uvuvi, kilimo yenyewe, fedha, elimu, viwanda ili kusudi tuweze kuipa kipaumbele sekta ya lishe au masuala ya lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo eneo la nishati, tumeona katika kurasa hizo za hotuba ya Mheshimiwa Waziri 23 – 25 kwamba kuna bilioni zaidi ya 400 zimeenda katika kuendeleza Sekta ya Nishati, lakini kuna tatizo moja ambalo naliona kwamba kiasi cha bilioni 400 haziakisi sana matatizo ya kukatikakatika kwa umeme. Tatizo hili ni kubwa na hasa tunapokwenda na sera yetu ya Tanzania ya viwanda tatizo hili linaweza likawa ni kikwazo kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana kwanza niwapongeze sana Waziri na Naibu wake wanafanya kazi nzuri sana katika sekta hii, wanajitahidi sana. Kila unapowaambia tatizo lolote wana-respond haraka na ni kwa dakika chache sana tatizo linakuwa limetatuliwa ila ninachoona TANESCO haina Watendaji wazuri. Baadhi ya Watendaji wa TANESCO kwa kweli wanatukwamisha. Kwa hiyo wapitie vizuri utendaji wa watumishi wa TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono asilimia mia moja.
Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa FAO wa Kuzuia Uvuvi Haramu kupitia Bandari za Nchi Wanachama pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Kuanzishwa kwa Ushirikiano wa Kimataifa wa Nishati ya Jua (The Framework Agreement on the Establishment of International Solar Alliance)
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja zetu za maazimio mawili. Kwanza, niseme naunga mkono hoja za maazimio yote mawili ambayo ni Azimio la Nishati ya Jua na Azimio la Mkataba wa Kimataifa wa FAO.

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia zaidi Azimio hili la Mkataba wa Kimataifa wa FAO. Nianze tu kwa kusema kwamba, Azimio hili linahusu sana vipengele vitatu, ambapo kimojawapo kinahusu illegal, ambayo ni uvuvi usiozingatia sheria na cha pili ni unreported na cha tatu ni unregulated. Sasa katika hiki cha tatu cha unregulated fishing, niseme tu kwamba, katika suala zima la udhibiti hatuwezi tukaepuka kufanya resource assessment, kama nchi.

Mheshimiwa Spika, huwezi ukadhibiti kama hujui una kiasi gani cha rasilimali au aina gani ya rasilimali ya mazao ya bahari. Kwa hiyo, naomba sana Serikali, katika kutekeleza suala zima la udhibiti, iweke nguvu zake katika utafiti ili kusudi tuweze kujua ni kiasi gani ambacho tunacho katika bahari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo hoja na dhana tofauti tofauti katika suala hili. Kwa sababu kuna wengine ambao wanasema kwamba, aina kubwa ya samaki bahari yetu kuu ni jodari; na hawa jodari wana-move sana, wana-move faster, hawakai katika eneo moja la nchi yetu. kwa hiyo siyo wetu. Pia, wanasema kwamba ufanyaji wa resource assessment ni kitu kigumu sana, lakini mimi niseme tu kwamba hii siyo hoja kubwa sana kwa sababu hata kama tutakuwa tumemsikia vizuri mchangiaji aliyetangulia, ametueleza wazi kwamba asilimia 70 ya jodari inatokea Mafia, katika eneo la Kitutia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni kwamba hawa samaki ni wetu na tuna kila sababu ya kufanya resource assessment. Hata ukiangalia katika mbuga yetu ya Serengeti, utaona kwamba wale nyumbu, pundamilia na wanyama mbalimbali huwa wana-move kutoka eneo letu la Tanzania na wanaenda Kenya, lakini resource assessment huwa inafanyika. Tunajua tuna kiasi gani cha nyumbu, tunajua tuna kiasi gani cha pundamilia na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili suala naomba Wizara isilikwepe, itilie maanani, iwezeshe vituo vyetu vya utafiti (TAFIRI) na hata Chuo chetu cha Mbegani ili waweze kushirikiana kufanya resource assessment, ndipo tutakapoweza kudhibiti vizuri.

SPIKA: Mheshimiwa Anastazia, nilitaka kukwambia tu, hawa nyumbu ambao wanazunguka Kenya, Masai Mara kurudi Tanzania na kurudi Kenya tena, zaidi ya 90% wanazaliwa Tanzania. Endelea tu namchango wako. (Makofi)

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa taarifa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo naependa nizungumzie ni kuhusiana hasa na faida kubwa ambayo tunapewa na huu mkataba. Tunapewa fursa kubwa sana na hasa kupitia ile United Nations Conversions on the Law of the Sea, ambapo kuna kifungu kimoja ambacho kinazitaka hizi nchi wanachama wahakikishe kwamba wanatumia rasilimali hizi za bahari wao wenyewe na ile ziada ndiyo wanawapa nchi nyingine na hasa kipaumbele kiwe kwa zile nchi ambazo hazina bahari.

Mheshimiwa Spika, hapa napenda tu kusisitiza kwamba Serikali yetu sasa inatakiwa iangalie suala zima la ustawi wa wananchi na hasa kwa kuzingatia upatikanaji wa samaki kama lishe kwa wananchi. Kwa kweli hili ni muhimu sana na hasa ukiangalia kwamba katika nchi yetu matumizi ya samaki ni madogo sana, lakini ni muhimu sana kuliko hata nyama na vyakula vingine. Samaki ni muhimu sana kwa afya, lakini tunatumia kilo karibu saba hadi kumi kwa mwaka na wakati mahitaji hasa yanatakiwa tupate takribani kilo 20 kwa mwaka. Kwa hiyo, tunachotakiwa sasa kufanya ni kuwawezesha wavuvi wetu wadogo waweze kupata hawa samaki kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wapate lishe bora.

Mheshimiwa Spika, kuna suala zima la Sheria ya DSFA pamoja na kanuni zake. Kumekuwepo na malalamiko ambayo tumeyashuhudia hasa kutoka Zanzibar, kwamba, kulikuwa na kanuni ambayo inawataka wale wavuvi waweze kuleta by-catch katika nchi husika. Wanapokuwa wamevua na kupata wale samaki ambao hawakuwa wamepewa ruhusa yake kuwavua, basi wawalete katika nchi husika. Sasa kilichokuwa kinatokea ni kwamba, wanawaleta wale samaki, halafu wanauza. Kwa hiyo, kilio kwa wavuvi ni kwamba bei ya samaki inashuka na wakati wao wametumia gharama kubwa katika kuvua.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kupendekeza hapa ni kwamba, hii Sheria ya DSFA pamoja na kanuni zake, irejewe ili kusudi suala zima la by-catch pale ambapo tutakuwa tumeziruhusu sasa meli nyingine za nchi za nje kuja kuvua samaki, suala la by-catch liwekewe utaratibu maalum ili kusudi wale wavuvi ambao wanavua karibu karibu waweze kuwapata hawa by-catch angalau waweze kushusha bei ya samaki kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, sheria au ule Mkataba wa UNCLOS unasema kwamba hawa by-catch ni mali ya nchi husika, siyo mali ya wale wavuvi wakubwa. Kwa hiyo, ni makosa makubwa sana wanapokuwa wakileta samaki halafu wanawauza wao wenyewe kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ningependa nisemee, unapofanya regulation au udhibiti, huwezi kuepuka suala zima la kuwa na bandari. Bandari ya Uvuvi ni lazima, lakini vilevile dry-dock, sijui inaitwaje kwa Kiswahili. Dry-dock ni muhimu sana ili kusudi kuweza kuzihudumia zile meli ambazo zinakuja pale. Badala ya kusema kwamba wanaenda nchi jirani, waende Mauritius au waende Kenya, basi wafanyie pale pale matengenezo ambapo inaweza ikahakikisha nchi yetu inapata kipato kikubwa ukichanganya pamoja na tozo za leseni na mambo mengine basi hata dry- dock inaweza ikachangia kukuza uchumi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia, kuwa mchangiaji wa kwanza jioni hii. Nashukuru sana na nitangulie kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi yake ya uhai na kwa mema mengi ambayo ametujalia katika Bunge letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kuwapa pole Watanzania wenzetu ambao wamekumbwa na maafa ya mafuriko na nimuombe pia Mwenyezi Mungu aiepushe nchi yetu na majanga ya aina hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuipongeza Ofisi ya Spika pamoja na Bunge letu kwa kazi nzuri ambayo tumeifanya jana ya kuwaenzi Maspika wastaafu. Kwa kweli ni kazi moja nzuri sana na ya kihistoria; naomba tujipongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa napenda pia kuishukuru Ofisi ya Spika kwa kuboresha vishikwambi, vimeboreshwa sana na vishikwambi hivi Kamati zetu zimeweza pia kutumia kwa kufanyia kazi za Kamati na vimefanya kazi nzuri sana. Na ukichukulia kwa mfano Kamati ya LAAC tulikuwa tunabeba vitabu vikubwa sana, vinaweza vikafika karibu kilo tatu au zaidi ambavyo vilikuwa vinatutesa sana, lakini kwa vishikwambi hivi sasa tumeepukana na hiyo adha, kwa hiyo tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuunga mkono taarifa za Kamati ya LAAC ambayo ni Kamati yangu, ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC, lakini pia Kamati ya PAC, naunga mkono taarifa zao, au taarifa zetu kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme ninachozungumza ninaongezea tu pale ambapo Kamati ya LAAC imezungumza kupitia Makamu Mwenyekiti wetu, kwa hiyo mimi ntaongezea kiasi fulani. Na nianze kusema kwamba katika maendeleo ya halmashauri au katika maendeleo ya Taifa kwa ujumla, cha kwanza kabisa ni lazima tuwe na rasilimali watu, lakini watu hawa tunaowasema ni lazima wawe ni watu wenye uwajibikaji wa kuridhisha. Lakini pia tunahitaji kitu kingine ambacho ni rasilimali fedha pamoja na vile vingine ambavyo alikuwa akivisema Hayati Baba wa Taifa; ardhi, siasa safi, uongozi bora, lakini mimi ntazungumzia hivi vitu viwili; rasilimali watu na rasilimali fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukienda katika halmashauri zetu tumekuwa na changamoto kubwa sana katika ukusanyaji wa mapato, na hili linatokana na baadhi ya watumishi kutokuwa waaminifu na vitu ambavyo vimekuwa vikitumika, zile nyenzo ambazo ni mashine za POS, watumishi hawa wamekuwa wakitumia POS bandia, mashine za POS bandia, lakini vilevile wakati mwingine wamekuwa wakizima data, na kuna wakati pia wanazitumia kwa matumizi tofauti na yale ambayo yamekusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu naipongeza sana Wizara ya TAMISEMI inayosimamiwa na Mheshimiwa Waziri Jafo na Naibu Mawaziri wake kwa uamuzi ambao wamechukua hivi karibuni. Uamuzi huu ni wa kuleta mashine mpya za POS ambazo zimeboreshwa vizuri sana. Mambo kama haya ambayo wamekuwa wakiyafanya hayawezekaniki katika mashine hizi mpya. Kwa hiyo, wameleta na wamesambaza mashine ambazo ni zaidi ya 7,000 katika halmashauri zote, mashine ambazo zimeboreshwa, ni za kisasa na zina identification yake kabisa, hawawezi wakatumia mashine bandia.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kikubwa zaidi niseme tu kwamba tunapaswa kumpongeza sana Mheshimiwa Jafo na ofisi yake kwa jinsi ambavyo wamepunguza gharama za kuleta hizi mashine. Wameleta mashine kwa gharama ya asilimia 30 ya ile gharama ambayo ilikuwa ikitumika mwanzoni kununua mashine hizohizo. Kwa hiyo, tunapaswa wote kujifunza na kuiga uzalendo huu ambao wenzetu wametumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo niseme tu hivi karibuni halmashauri nyingi zimepunguza uwezekano wa kuwa na hati chafu, halmashauri zenye hati chafu ni chache sana. Lakini nitahadharishe tu kwamba kuwa na hati safi haimaanishi kwamba halmashauri zenye hati safi ndizo zinazofanya kazi nzuri kimaendeleo; hii si kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii inatokana na nini; ni kutokana na mfumo wetu wa ukaguzi wa miradi ya maendeleo kwa sasa. Tunachokagua, unakuta tunakagua input na output, lakini performance audit tumeiacha, impact hatuiangalii sana. Kwa hiyo, tunakwenda kwenye input ambayo kwa Kiswahili nimetafuta sana Kiswahili chake, tulihangaika sana kwenye Kamati lakini nimepekuapekua nikakuta input ni pembejeo, ila sio pembejeo za kilimo. Ukisema input ina maana ni pembejeo, na output ni pato ila sio mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunakwenda kwenye input-output, ikiwa na maana kwamba kama unajenga kituo cha afya umeweka input pale ambazo ni fedha, na output ni kituo cha afya. Sasa tunashindwa bado Ofisi ya Mkaguzi inahitaji kuimarishwa zaidi ili iweze kufanya performance audit. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwa uchache kutolea mfano mradi mmoja wa maji; unaweza usiamini kwamba tuna engineer wa maji ana-design mradi lakini ana-skip ile hatua ya kufanya water treatment, na mradi huu unaripotiwa kwamba umekamilika. Lakini ukishafika kwenye mradi sasa kuangalia performance au impact ya ule mradi, wananchi hawachoti maji pale badala yake wanaendelea kuchota maji katika visima binafsi, tena kwa kununua. Kwa hiyo, hapa ndipo mahali ambapo naona kuna gap, na kwa sababu hiyo niombe sana Ofisi ya Mkaguzi Mkuu iwezeshwe ili iweze kufanya performance audit. Ni kengele ya kwanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, utakuta pia – pengine itakuwa ni makusudi ana-skip hii hatua. Na miradi mingi tumeikuta hivyo, ni Kamati tumekwenda na tumekuta mambo kama hayo. Sasa wana-skip baadhi ya hatua, lakini baadaye kuna kichochoro fulani, kichaka tuseme, cha kuibia fedha, wanaweka variation kuongeza fedha na zile fedha unakuta ni nyingi sana, na kwa sababu hiyo sasa ndipo ubadhirifu ambapo unatokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nisingependa niongee mengi sana lakini pia niombe hata kwenye vituo vya afya tuangalie suala la kuboresha hivi vituo vya afya viendane na kupunguza vifo vya akina mama na watoto. Kwa sababu kituo cha afya ni jambo moja lakini impact au ile athari ndiyo tunayoitaka hasa. Sasa tatizo ni ule usimamizi wa wale wahusika katika yale maeneo; waganga wakuu wa wilaya, waganga wakuu wa mikoa, sidhani kama wanafanya usimamizi wa kutosha kwa sababu ukiangalia takwimu utakuta kwamba kazi imefanyika kubwa, fedha zimetumika nyingi lakini vifo vya akina mama na watoto viko palepale katika baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia jioni hii. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyenzi Mungu kwa wingi wa neema na rehema zake ambazo anatujalia kila iitwapo leo.

Kwa namna ya pekee kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Mpango - Waziri wa Fedha pamoja na Naibu wake - Mheshimiwa Dkt. Kijaji wakisaidiana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri ambayo wameifanya ya kuandaa vizuri sana mapendekezo ya bajeti ya Serikali kwa weledi mkubwa na niseme tu kwamba bajeti hii au mapendekezo haya yamezingatia maslahi ya Taifa na imegusa maslahi ya makundi mbalimbali hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nianze kuchangia kwa kuzungumzia suala la maji kwa Mkoa wa Mtwara kwa bahati nzuri nimepata taarifa kwamba Mheshimiwa Prosfesa Mbarawa alikuwepo Mtwara wiki iliyopita na amefanya kazi nzuri ya kukagua utekelezaji wa miradi katika mkoa wa Mtwara ukiwepo Mradi wa Makonde ambao unagharimu kiasi cha dola milioni 70. Nimshukuru sana Mheshimiwa Mbarawa lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu hii ahadi yake aliyoitoa wakati alipotembelea Mkoa wa Mtwara mwezi wa nne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee tena naomba niishukuru Serikali kwa upandea wa afya mkoa wetu wa Mtwara umeweze kupatiwa shilingi bilioni 10.3 kwa ajili ya kujenga vituo vya afya 13 pamoja na hospitali za Wilaya tatu. Lakini napenda niifahamishe sasa Serikali kwamba baadhi ya vituo vya afya vimekamilika. Lakini havijaanza kutumika kutokana na ukosefu wa vifaa tiba pamoja na wataalamu wa kuhudumia vile vifaa. Kwa hiyo, naomba nitoe ombi langu kwa Serikali iweeze kututekelezea au kututimizia haya mahitaji ili kusudi vituo hivi viweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande huo huo wa afya naomba nizungumzie kwa uchache kabisa suala la vifo vya uzazi. Ukingalia takwimu za kitaifa utaona kwamba kuna vifo kwa wastani wa 500 kati ya vizazi hai 100,000 kwa kitaifa. Lakini nilipokwenda Mkoa wa Mtwara kuangalia takwimu nimepata kwamba vifo ni kuanzia mwaka 2015 ni 168; mwaka 2016 ni 146; mwaka 2017 ni 148 na mwaka 2018 ni 245 na hii kati ya vizazi hai 100,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ukiangalia utaona kwamba hii iko chini ya wastani wa kitaifa jambo ambalo ni jema. Lakini sasa hii trend ukiangalia vizuri utaona haipo reliable na wala haipo predictable.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe Wizara ya Afya iende kufanya utafiti kwa undani kwamba ni maeneo gani ya nchi yetu yanapekea vifo hivi au hizi takwimu za kitaifa kuwa juu kufikia 500 au zaidi. Lakini pia iangalie na sababu zinazopelekea vifo hivi kufikia juu, nitoe mfano tu mwaka 2015 katika Hospitali ya Wilaya Mkomaindu waliweza kunipa sababu ya vifo vingi katika Hospitali hiyo ya Rufaa ukilinganisha na Kituo cha Afya cha Nanyumbu kwa wakati ule Nanyumbu ilikuwa ni kituo cha afya kabla haijapandishwa hadhi. Walisema kwamba vifo hivi vinachangiwa kwanza umbali wa kutoka kituo cha afya na ni kwa sababu kwamba wakina mama wengi wanapata rufaa kutoka Nanyumbu na wanapekwa pale wakiwa katika hali ambayo si nzuri, wanakuwa na complications fulani, kwa hiyo ndio maana wanakuwa na vifo vingi ukilinganisha na Kituo cha Afya cha Nanyumbu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwaka jana 2018 pia niliweza kufuatilia Hospitali ya Ligula na Likombe. Data zao zilionesha kwamba katika Hospitali ya Ligula vifo vya akina mama vilikuwa ni vingi ukilinganisha na Kituo cha Afya cha Likombe. Kwa hiyo, niombe tu kwa sababu pale sikupata sababu nini niombe sasa Serikali ingalie maeneo kama haya ili iweze kupanga mkakati madhubuti wa kukabiliana na haya matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijamalizi mchango wangu ningependa kuishukuru sana Serikali na kuipongeza kwa kuweka mazingira wezeshi ili kuweza kuleta mageuzi ya kiuchumi katika halmashauri zetu na kwa wananchi kwa ujumla. Niseme kwa mfano kuna upanuzi wa bandari ambao unaendelea kule Mtwara, lakini vilevile kuna ujenzi au ukarabati wa uwanja ndege huko huko Mtwara. Niseme tu kwamba shughuli hizi ambazo zinafanywa zitaweza kuzisaidia Halmashauri zetu na Mkoa wetu kwa ujumla kuongeza njia mbalada za kuongeza kipato badala ya kutegemea zao la korosho pekee.

Kwa hiyo, nishukuru sana Serikali lakini hapo niongezee tu kwamba kuna mwenzetu mmoja hapa alikuwa akisema kwamba wananchi wawezeshwe kuanzisha viwanda wa ngozi na kadhalika na kadhalika. Lakini sasa tukirudi nyuma tujiulize kwamba kati ya kuku na yai kinaanza kitu gani. Sasa ni lazima kwanza yawekwe mazingira wezeshi, ujenzi wa miundombinu, ujenzi wa umeme ambao unaaminika na wa gharama nafuu ni vitu vya muhimu sana kuwepo ili wananchi waweze kuvitumia kwa ajili ya kuzalisha kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kusema kwamba Mkoa wa Mtwara una vivutio vingi sana ambavyo mazingira haya wezeshi yanaweza yakasaidia katika kukuza utalii kwa mfano ukienda unakuta kuna Shimo la Mungu kule Newala, kuna Mji Mkongwe wa Mikindani, kuna Makonde Plateau, lakini pia kuna beach nzuri sana, kuna mmoja amezungumzia hapa utalii wa pwani. Kwa hiyo, utalii unaweza ukasaidia kuwa kama ndio njia mbadala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuiomba Serikali hasa Waziri wa Elimu kwamba mambo ni mengi ambayo yamefanyika katika nchi yetu, makubwa sana katika awamu hii ya tano, sasa tusiishie kusifia nakupongeza lakini Waziri wa Elimu nimuombe akae na timu yake ya watalam ili waone ni namna gani wanaweza wakayaweka masuala haya yote makubwa na ya kihistoria katika system yetu ya elimu ili kusudi tuweze kurithisha vizazi vijavyo ambao nao wanaweza wakajengewa uzalendo kutokana na mamba haya haya wakawa wazalendo wa kweli, vilevile wakawa majasiri, lakini wakajenga uthubutu kupitia masuala haya muhimu na makubwa ya kihistoria ambayo yameweza kufanyika. Nadhani hakuna haja ya kuyataja sote tunayafahamu ni mambo mazuri nadhani tuanze sasa ili kusudi tuweze kujenga kizazi kijacho ambacho kinaweza kikayatumia masuala haya kuleta maendeleo katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijamalizia niombe kukumbushia Ofisi ya Waziri Mkuu kwamba walituahidi wataleta sheria ambayo itasaidia kutenga fedha katika Halmashauri kwa ajili ya lishe ya watoto wa chini ya miaka mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mmoja ya wachangiaji kwa siku hii ya leo.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa neema na rehema zake ambazo amekuwa akitujaalia kwa kila iitwapo leo lakini zaidi sana, napenda sana kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Rais wa Zanzibar pamoja na timu yote ya Mawaziri kwa jinsi ambavyo wamekuwa wakitekeleza vizuri na kwa uzalendo mkubwa na kwa umahiri Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Wajumbe wote wa Kamati kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi kwasababu wao wamekuwa wakisimamia kwa ukaribu sana utekelezaji huu wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na kwa namna ya pekee nimshukuru sana Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Dkt.Bashiru Ally kwa namna ambavyo amekuwa akituongoza vizuri katika chama chetu lakini pia kwa jinsi ambavyo amekuja Mkoani Mtwara mwezi uliopita na amesimamia vizuri, amekagua miradi ambayo imekuwa ikitekelezwa. Kwa hiyo, nampongeza na namuomba aendelee na moyo huo.

Mheshimiwa Spika, nichukue pia nafasi hii kukushukuru na kukupongeza sana kwa kazi nzuri ambayo unaifanya na niseme hili suala la E-parliament limekuja kwa wakati muafaka kwa sababu nilikuwa najiuliza hapa kwamba ingekuwa ni wakati ule wa kuhangaika na makabrasha sijui kama kuna mtu ambaye angeweza kusoma makabrasha yale kwa sababu kila mmoja angekuwa anogopa kupekuwapekua. Kwa hiyo, nimuombe Mwenyezi Mungu akubariki sana wewe na Naibu Spika, Katibu wa Bunge pamoja na timu yako kwa jinsi ambavyo mmekuwa mkitujali na kuwa na maono ya kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Mtwara; Wananchi wa Mkoa wa Mtwara wamenituma nilete shukurani zao za dhati kwa jinsi ambavyo Serikali yetu ya Awamu ya Tano imekuwa ikiwasaidia na ikiweka jitihada katika kuwainua kimaendeleo na kwa kuanzia tu niseme; katika maendeleo ya miradi ya maji tunakwenda vizuri. Manispaa ya Mtwara sasa hivi imefikia hatua ya kupunguza kwa kiasi kikubwa sana mgao wa maji na sasa iko katika hatua za kutengeneza chujio la maji kule Mtawanya.

Mheshimiwa Spika, pia kuna mradi wa Mkwiti ambao una lots tatu; lots mbili ziko katika hatua za utekelezaji lakini kuna lot moja ambayo imebaki na naiomba Serikali sasa iongeze kasi ili kusudi wananchi wa Tandahimba na Newala waweze kupata maji kwa sababu mradi huu wa maji ya Mkwiti utatumika pale lot ya tatu itakapokuwa imekamilika.

Mheshimiwa Spika, nishukuru pia kwa upanuzi wa uwanja wa ndege ambao unaendelea kule Mtwara, lakini pia upanuzi wa bandari ujenzi wa hospitali ya rufaa ya kanda na ujenzi wa hospitali za wilaya pamoja na vituo vya afya ambavyo vinaendelea na vitatusaidia sana kuhakikisha kwamba afya ya wananchi wa Mtwara inaboreka.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa namna ya pekee, nishukuru sana sana kwa ujenzi wa barabara ya uchumi ambao unaendelea kwa sasa, lakini kwa upande huu niiombe Serikali pia iongeze kasi kwa sababu bado kidogo naona kilometa ambazo zimekuwa covered ni chache, lakini naamini kabisa katika bajeti hii tutakuwa tumepiga hatua kubwa.

Mheshimiwa Spika, kama walivyosema wenzangu kuhusiana na ugonjwa wa corona, nami niungane na wenzangu wote kutoa mchango wangu katika eneo hili. Sidhani kama kuna mtu ambaye atakataa kwamba ugonjwa huu hauna dawa ugonjwa, hauna dawa na kilichobaki, ni kumwomba Mwenyezi Mungu. Hili tukimwachia Mwenyezi Mungu naamini kabisa atatusaidia kama alivyotusaidia kutuokoa kwenye kimbunga kilichotokea mwaka jana ambapo hakuna ambaye alitarajia kimbunga kile kisingeweza kutupata, lakini ni kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu kimbunga kile kiliyeyuka bila kutarajia.

Kwa hiyo, naamini kabisa kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu atatuepusha na janga hili, kwa hiyo, ni wajibu wa kila mmoja wetu kusali na kumwomba Mwenyezi Mungu atuepushe na hili janga laini pia atusamehe popote pale ambapo tumemkosea kwa namna moja au nyingine.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mchango wangu kidogo, Waziri Mkuu ametuambia kuwa, kuna kamati tayari imeshaundwa ambayo inakutana. Sijui wajumbe wa Kamati hii pamoja na kwamba ametuambia ni Mawaziri na wataalam kutoka sekta mbalimbali, lakini napendekeza kwamba tungekuwa na wataalam wa lishe waliobobea ambao wangeingia kwenye Kamati hii, lakini na wataalam wa micro biology, naamini kabisa tunao. Kwa hiyo, wataalam hawa kwa mfano kwa upande wa lishe, ukiangalia clips nyingi sana watu ambao wamekuwa wakishambuliwa na huu ugonjwa wanajitibu kutokana na vyakula.

Mheshimiwa Spika, lakini vyakula hivi vina kazi kubwa sana ya kuzuia nikiwa na maana kwamba kuna kuwa na zile contents ambazo zinakuwa na uwezo mkubwa wa kutoa kinga dhidi ya maradhi ya virus, kwa mfano wengi wamekuwa wakitaja kwamba wametumia machungwa, malimao, tangawizi na vyakula hivi kwa kifupi tuseme ni vile vyakula ambavyo vinakuwa na zinc na vitamin C. Sasa ukiangalia tabia ya zincm ina kazi kubwa sana ya kusaidia kinga ya mwili dhidi ya maradhi mbalimbali. Kwa hiyo niombe tu kwamba wale wataalam wa lishe watatusaidia sana sana kutushauri kwa mfano, katika matumizi ya tangawizi, vitunguu swaumu, mbegu za maboga maziwa korosho na watatuelekeza mazao mengi ambayo yanatoa hivi vitu ambavyo vinatusaidia katika kuongeza kinga ya mwili.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kidogo suala la mafuriko. Suala hili ni matokeo ya mabadiliko ya tabia nchi na limekuwa likisumbua sana kwa muda mrefu, kwa hiyo, ni ushauri wangu sasa Wizara ya Ujenzi ikae na kuangalia ule mpango ambao nchi yetu uliweka katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi na Wizara ambayo inahusika na ujenzi ikae iangalie ni mambo gani ambayo imeyaruka ili kusudi iweze kuyajumuisha katika mpango wa kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi. Nimekauka koo, ahsante sana.

SPIKA: Watakuletea maji, watakuletea maji muda si mrefu.

MHE.ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, haya ahsante nasikia kukauka koo sijui ni kwa nini. (Kicheko)

SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa Anastazia Wambura.

MHE.ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia jioni hii.

Mheshimiwa Spika, nimeomba maalum kwa ajili ya wananchi wa Kata ya Mayanga katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara na ni kuhusu malalamiko makubwa ambayo yanatokana na uchafuzi wa mazingira unaotokana na Kiwanda cha Simenti cha Dangote. Nitakwenda moja kwa moja, labda kama muda utaruhusu basi naweza nikaongea jambo lingine.

Mheshimiwa Spika, haya ni malalamiko ya muda mrefu na kwa taarifa ambazo nimezipata ni kwamba hata NEMC walishawahi kufika Dangote pale na waliwaandikia barua ili waweze kurekebisha hiyo hali. Kiwanda hiki cha Dangote ni kiwanda ambacho kipo katika Kata ya Mayanga, Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara.

Mheshimiwa Spika, mwanzoni wakati hiki kiwanda kinajengwa, tuliambiwa kwamba kutakuwepo na mechanism ambayo itakuwa inazuia zile pollutants kufika kwenye mazingira ya wananchi. Kwa bahati mbaya sasa, mwanzoni kilipoanza tukawa tunapata taarifa kwamba, nyakati za usiku unatoka moshi na vumbi lingi sana, tena wanasubiri nyakati za usiku ndipo hali hii inatokea, lakini imeendelea hivyo na baadaye sasa tunaona hata mchana hali hii inajitokeza.

Mheshimiwa Spika, sasa NEMC kwa taarifa hizo ni kwamba wameshapeleka barua Dangote, lakini mpaka sasa bado hali ni ileile. Kwa bahati mbaya ni kwamba wananchi wanapoona hali inazidi kuendelea wanaamua kwenda pale Dangote ili waonane na uongozi, lakini bahati mbaya tena zaidi ni kwamba wanazuiliwa getini, hawawezi kuonana na uongozi.

Mheshimiwa Spika, ni ombi langu kwamba Waziri, Mheshimiwa Jafo pengine na Naibu wake, walifanyie kazi hili. Wafike pale waonane na wananchi ili waweze kuwaeleza hali halisi. Hata hivyo, naomba zaidi sana hatua za haraka zichukuliwe ili kuweza kunusuru mazingira haya ambayo yanachafuliwa. Kwa kweli hali ni mbaya sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda unaruhusu, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan, kwa kupata nafasi ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mujibu wa Katiba. Nimpongeze sana kwamba jana tumesikia ametoa msamaha kwa wafungwa 5,000 na hii ina implication kwenye mazingira ya Magereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tumpongeze sana kwa sababu wafungwa wanaposongamana magerezani inaharibu pia mazingira ya magerezani na kuharibu pia afya zao. Kwa hiyo tunamshukuru sana na tunampongeza kwa kufanya jambo hili.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze pia…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Wambura anasema Mheshimiwa Rais amesamehe wafungwa, siyo wale waliofungwa juzi pale Uwanja wa Benjamin Mkapa, hapana; wafungwa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Wambura, endelea, nilikuwa nasisitiza unachokisema.

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kutoa ufafanuzi; ni kweli wengine wasingeweza kunielewa.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia kumpongeza sana Dkt. Philip Mpango kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kuwa Makamu wa Rais na kwa kupitishwa kwa kura nyingi sana na Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Jafo na Naibu wake; tumewaona wakipita katika maeneo ya machimbo na kusisitiza hali ya kuzuia uchafuzi wa mazingira. Kwa hiyo naomba waendelee na kasi hiyo.

Mheshimiwa Spika, kama muda upo, nizungumzie kidogo kuhusiana na mabadiliko ya tabianchi ambapo tunaona sasa hivi mafuriko yanatokea mara kwa mara, wakati mwingine pia madaraja, barabara zinakatika. Nitoe mapendekezo kwa Serikali, mipango miji; tumezoea kuona wenzetu wa mipango miji wanatandika jamvi la viwanja. Inaweza ikatoka wilaya moja hadi nyingine, hakuna nafasi hapo katikati ya kuruhusu water sinks.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nipendekeze kwamba, wanapopanga mipango miji na kukata viwanja basi wawe na tabia sasa ya kuona kwamba mafuriko yanaweza yakatokea, kwa hiyo waache sehemu ambazo mvua zikinyesha zitapokea maji kwa sababu sehemu kubwa itakuwa imefunikwa na mapaa ya nyumba.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa miundombinu tubadilishe sasa standards tuongeze viwango vya barabara zetu, viwango vya madaraja, ili yaweze kuwa imara kuhimili mafuriko.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, napenda kutoa hongera sana Waziri Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Mollel kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara ya Afya. Pia hongera kwa Mheshimiwa Rais Mama Samia kwa kuongeza idadi ya vituo vya afya katika nchi yetu kwa muda nfupi.

Mheshimiwa Spika, nina ushauri katika eneo la upatikanaji wa dawa, ufanyike ukaguzi wa kushtukiza katika vituo vya afya mara kwa mara ili Wizara iweze kujua ukubwa wa tatizo na kuwabaini wanaofanya ubadhirifu katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, miongozo ya Wizara ya utoaji dawa katika vituo vya afya ipitiwe upya na kuangalia ile inayogongana na ya NHIF na kuiweka sawa ili kuondoa usumbufu wakati wa madai ya fedha ya vituo vya afya na NHIF.

Kuhusu huduma bure kwa akina mama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano itolewe maelezo ya kubainisha hiyo bure inahusisha vitu vipi au gharama zipi ili ieleweke wazi kwamba Serikali inahusika katika maeneo yapi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni hii. Nianze kwa kukupongeza wewe pamoja na Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuaminiwa na Kamati Kuu, lakini pia kwa kupitishwa kwa kishindo na Bunge lako hili Tukufu. Nimwombe Mwenyezi Mungu aendelee kuwasimamia na kuwaongoza katika majukumu yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipongeze pia CAG pamoja na ofisi yake kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya, lakini pia nadhani wajumbe wa Kamati ya LAAC, PAC na PIC wanafahamu namna ambavyo mafunzo yake yametusaidia na sasa tumekuwa kama ni ma-CAG wadogo. Niwapongeze pia Wenyeviti wetu wa Kamati hizi mbili, wame-present vizuri sana hoja za Kamati. Kwa hiyo nimesimama hapa kuunga mkono hoja za Kamati zote, hizi mbili kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa na machache sana ya kuongezea katika taarifa ya LAAC. Nianzie na ubora wa majengo; kwa mujibu wa taarifa ya CAG tumekuwa tukipata taarifa mara kwa mara na hasa kwa hii taarifa ya mwisho aliyoileta CAG, kuna baadhi ya majengo ambapo akikagua utakuta kuna nyufa katika kuta na katika sakafu na hii haileti afya katika matumizi ya fedha za umma.

Mheshimiwa Spika, ukichunguza sana utakuta sababu mojawapo ni kwamba baadhi ya halmashauri hazina Wahandisi wa kutosha, lakini hata wale Wahandisi ambao wapo wanakuwa hawana vitendea kazi, kwa mfano, usafiri. Kwa hiyo utakuta kwamba, hasa kwenye hii miradi ambayo inatumia force account, kwa kweli ni shida kwa sababu wanajenga tu wale mafundi ambao wameaminiwa, lakini Wahandisi wetu wanapokuwa wakihitajika kukagua, hawana usafiri, kwa hiyo hawafiki pale kwa wakati. Unakuta order imetolewa kwamba tunataka ndani ya mwezi mmoja wanafunzi wawe wameshaingia darasani, kwa hiyo wanaamua tu leo ameweka msingi, anapandisha tofali, moja kwa moja anaendelea lenta na kupaua, kwa hiyo yanakuja kutokea madhara kama hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitoe ushauri tu kwa Serikali kwamba sasa ihakikishe kwamba kunakuwa na Wahandisi wa kutosha, lakini vile vile wapatiwe vitendea kazi kama usafiri ili waweze kwenda kwa wakati, wafanye ukaguzi kwa wakati na vilevile kutoa ushauri ili kuweza kupata majengo yenye ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee kidogo tena hoja yangu ya pili ambayo ni ya mikopo ambayo inatokana na asilimia kumi ya fedha za ndani kwa ajili ya wanawake, vijana na wenye ulemavu. Niseme tu maswali ya jana na leo katika eneo hili ni indication tosha kabisa kwamba kuna tatizo katika eneo hili la mikopo. Tatizo lipo na panahitajika ufuatiliaji wa karibu.

Mheshimiwa Spika, zipo halmashauri ambazo zinafanya vizuri katika eneo hili kwa upande wa marejesho ya mikopo na utakuta kuna wengine wanaorodhesha vizuri kabisa kwamba mikopo iliyorejeshwa kuna kiasi kadhaa ambacho kimepelekwa tena kwenye vikundi vingine. Hata hivyo, kuna baadhi ya halmashauri ambazo zinahitaji uangalizi na ufuatiliaji wa karibu kabisa ili kuweza kujua hizi fedha ambazo zimerejeshwa zinakwenda wapi na zinakopeshwa vipi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe tu Ofisi ya CAG kwa sababu mpaka sasa hakuna utaratibu wa kuzikagua hizi fedha ambazo zimerejeshwa, hatujaona utaratibu huu. Kwa hiyo niombe Ofisi ya CAG ifanye ukaguzi kuangalia hizi fedha ambazo zimerejeshwa zinakopeshwa na zinakopeshwa kwa namna gani na atoe taarifa ili kusudi Kamati iweze sasa kupata msingi wa kuhoji hizi halmashauri na kujua nini kinachoendelea. Niombe pia mamlaka husika itoe format katika halmashauri, namna bora ya kuweza kuzitolea taarifa hizi fedha ambazo zimekopeshwa.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa halmashauri niombe halmashauri zijifanyie tathmini zenyewe, je, hii mikopo wanayotoa ina tija? Niseme tu kwamba, kama mikopo hairejeshwi, ina maana kabisa na ni indication moja wapo kwamba hakuna tija katika hii mikopo.

Mheshimiwa Spika, kimsingi tuna watumishi wa aina mbalimbali katika halmashauri kuna Maafisa Biashara, lakini utakuja kushangaa kwamba, unaona wanawake wengi na vijana na watu wenye ulemavu, ambao wamekopa wanajikita kwenye biashara za uchuuzi wa bidhaa ya aina moja katika eneo moja na utaona kwamba hawafuati zile principle za demand and supply na matokeo yake ni kwamba wanakosa wateja na mwisho wa siku wanakuwa wameshindwa kurejesha mikopo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, naomba niseme tu kwamba niombe halmashauri zetu ziwe intergreted, zishirikiane ili kusudi kuweza kuwasaidia hawa wanaochukua mikopo tuweze kutimiza malengo ambayo tunayakusudia katika utoaji wa hii mikopo.

Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni hii. Pamoja na kumshukuru Mwenyezi Mungu, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na Ofisi yake kwa maandalizi mazuri ya hotuba ya bajeti ya ofisi yake, lakini pia kwa kuiwasilisha vizuri kwa umahiri mkubwa. Pia naipongeza sana Serikali yetu ya CCM ambayo inaongozwa na mama yetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa utekelezaji mzuri wa miradi ya maendeleo kwa njia jumuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia ujenzi wa uboreshaji wa miundombinu katika sekta ya elimu, sekta ya afya, sekta ya maji, barabara, na kadhalika, lakini hivi karibuni pia tumeshuhudia jinsi Maafisa Ugani ambavyo wamewezeshwa kwa kupewa vitendea kazi. Ni jambo jema na la kupongeza sana. Nampongeza pia Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa kazi nzuri. Tumeona wakulima wamepewa matumaini makubwa sana ya kuwezeshwa kwa kupewa pembejeo kwa mfumo wa ruzuku, tunaishukuru sana Serikali yetu. Naomba nitoe ushauri kidogo tu kwa upande wa kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mwelekeo mzuri wa utekelezaji wa kiujumla katika sekta ya kilimo, nasi sote ni mashahidi, lakini pamoja na jitihada zote hizi, mkulima kwa mfano wa korosho anazalisha korosho, lakini utaona kwamba, korosho hii haitumii vizuri ipasavyo, pamoja na kwamba, ni mzalishaji wa korosho. Ninasema haitumii ipasavyo kwa sababu ulaji wa korosho kwa kweli kwa Mtanzania ni kidogo sana. Ukichukulia kwa mfano wa nchi kama ya India, ni ya tatu duniani kwa uzalishaji wa korosho. Inazalisha zaidi ya tani 700,000. Tanzania inazalisha zaidi ya tani 200,000, lakini ukiangalia kwa matumizi ya korosho, India inatumia korosho zaidi ya tani 300,000 wakati Tanzania sisi hatupo hata kwenye ramani ya utumiaji wa korosho. Tunatumia korosho kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kutokutumia mazao ambayo anazalisha mkulima, hasa yale ya chakula, tutaona pia bei inashuka mara kwa mara na kwa kiasi kikubwa; na utakuta hata kila mwaka bei inashuka, lakini zaidi ya hapo, maisha ya mkulima yanaendelea kuwa duni. Hakuna tafsiri ya moja kwa moja ya uzalishaji wake na uboreshaji wa maisha yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitoe ushauri kidogo tu kwamba, Serikali ifanye integration ya kilimo na viwanda. Nasema hivi ili tuweze kupata multiplier effect. Kwa mfano, suala la ajira limezungumzwa sana hapa, tuweze kupata pia mapato, tuweze ku-regulate pia bei. Kwa mfano, bei ya korosho; tukiwa na viwanda vyetu vya korosho kwa ajili ya kusafirishwa nje ambayo ni ghafi, itapungua na hii itasababisha mvutano; demand and supply principle pale, bei itapanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vya korosho vipo vingi sana katika nchi yetu, vipo. Kwa mfano watu binafsi wana viwanda 39 vya korosho; lakini ukiangalia ni viwanda 20 tu ndivyo vinavyofanya kazi. Sasa hii inashangaza. Utaambiwa kwamba, vile viwanda 19 ambavyo havifanyi kazi, havina changamoto ya mtaji, wala havina changamoto yoyote. Nami naiomba Serikali iangalie na kuchunguza ni kwa nini lile lengo la kubangua korosho ghafi 56,000 halikutekelezwa, inakuja kubanguliwa 9% tu? Inategemewa kubanguliwa korosho tani 4,900 kwa kipindi cha mwaka 2021/ 2022, tatizo ni nini hapa?

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali iliangalie hili kwa umakini kwa sababu suala la viwanda tumekuwa tukilizungumzia muda mrefu, hususan, viwanda vya korosho. Tumezungumza mara tumesema vibinafsishwe, mara vianzishwe viwanda, leo wanaanzisha watu viwanda 39 viwanda 19 visifanye kazi bila sababu yoyote ambayo inaelezwa hapa! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kilimo labda nimalizie tu kuiomba sasa Serikali ihimize utumiaji wa vile ambavyo tunavizalisha, hususan kwenye korosho. Korosho ina lishe, ina ubora mkubwa sana kwenye upande wa lishe, tutumie korosho Watanzania, ina manufaa makubwa sana hasa kwenye ku-control diabetes, pressure na magonjwa mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niingie kwenye upande wa afya. Tuna hospitali inajengwa kule Mtwara inakaribia kukamilika, hospitali ya rufaa ya Kanda ya Kusini ambayo iko Mitengo. Hii hospitali imekamilika kwa hatua za kwanza, lakini ina matatizo ya watumishi, inahitaji watumishi takribani 400 kwa hatua za kwanza ambapo ikikamilika itahitaji watumishi 1,200, lakini kwa sasa ina watumishi 46 tu ambapo madaktari bingwa ni wawili na madaktari wa kawaida ni watatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba maprofesa wale ambao wanastaafu na madaktari bingwa, waajiriwe angalau kwa mkataba katika hospitali hii na hata katika hospitali nyingine Tanzania, kwa sababu hili siyo tatizo la hospitali hii moja tu, ni katika maeneo mengi. Hata hivyo, naomba retirement age ikiwezekana iongezwe kwa sababu hili ni tatizo ili kusudi tuweze kukabiliana nalo. Mimi niko Kamati ya LAAC tunazunguka na tunaona shida ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongezee tu kidogo hapa kwamba, kuna tatizo pia katika hiyo hospitali. Maji yanayokwenda pale ni ya chumvi na wataalam wanasema itachukua muda mfupi sana vifaa kuharibika; na hakuna bajeti tena ya kutoa maji katika mradi mwingine. Kuna chanzo cha Mchuchu pale Mikindani kina maji baridi.

Sasa naomba Waziri wa Maji aangalie uwezekano wa kutoa maji ya baridi kutoka chanzo cha Mchuchu ili kusudi kupeleka pale kuzuia tatizo ambalo linaweza likajitokeza la kuharibika kwa vifaa katika ile hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu kwa kuomba uboreshaji wa miundombinu ya maji uende kwa kasi kubwa zaidi ya hivi ilivyo sasa, uende kwa kasi kubwa ambayo itazidi ongezeko la watu…

(Hapa, kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: …kwa sababu hili ni tatizo kubwa. Kwa mfano, Kisasa kule maji hatupati, tunachukua wiki mbili kupata maji.

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, kwanza napongeza kazi nzuri ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ya uboreshaji miundombinu ya elimu na uboreshaji wa bajeti ya elimu. Nampongeza pia Waziri Mheshimiwa Profesa Mkenda, Naibu Waziri Mheshimiwa Kipanga, Katibu Mkuu Profesa Nombo na wataalam wote wa Wizara kwa jinsi wanavyoendelea kuipaisha sekta ya elimu hususan kwa kufanya maboresho ya sera ya elimu na mitaala.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwanza suala la elimu ya awali lizingatiwe na kujumuishwa kama ni elimu ya lazima kwani hapa ndipo sehemu muhimu ya kumjenga mtoto.

Pili, kuna tatizo kubwa la uhaba wa walimu katika nchi yetu lakini vibali vya ajira ni vichache. Nashauri Serikali yetu ifanye kila liwezekanalo idadi ya walimu iongezeke kwani zipo shule zina madarasa ambayo hayatumiki kutokana na uhaba wa walimu.

Mheshimiwa Spika, tatu, wakati elimu ya amali itakapoanza ni vyema Serikali ikatumia mfumo wa PPP ili kuweza kupata mazoezi ya vitendo kwa wanafunzi wetu kutoka sekta binafsi. Kwa mfano wanafunzi wataweza kwenda katika garage, hoteli, maduka, vituo vya ushonaji nguo, mashambani na kwingineko ili kujionea na kushiriki kufanya shughuli husika kwa vitendo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nimshukuru pia Mwenyezi Mungu kwa rehema zake. Nianze mchango wangu moja kwa moja kwa suala zima la ukuaji wa kilimo katika nchi yetu. Suala la ukuaji wa kilimo limekuwa gumu kwa muda mrefu na niseme tu sababu kubwa sana ambayo imechangia shida ya ukuaji wa kilimo ni kuongeza maeneo ya kilimo, lakini hatuangalii vizuri suala la productivity ambalo ni production per unit area.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesikia pia hapa Serikali au Wizara ina mpango wa kuongeza eneo la umwagiliaji na niombe sasa kwa kuwa bajeti imeshaongezeka ijikite zaidi kwenye suala la productivity kwa sababu kwa bajeti hii sasa tunaweza kuwa na mbolea na tumesikia pia tutakuwa na mbegu bora, huduma za ugani zimeshaimarishwa na kadhalika. Kwa hiyo niombe Serikali sasa ijikite kwenye productivity.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye utoshelevu wa chakula. Tumesikia mara kadhaa kwamba kuna dalili kwamba Bara zima la Afrika litakuwa na shida ya utoshelevu wa chakula, lakini sana kwa upande wa kwetu ngano tunaona kwamba ina upungufu mkubwa na kwa takwimu tumesikia kwamba mahitaji ya ngano katika nchi yetu ni tani milioni moja na wakati huo huo sisi tunazalisha tani 70,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli tunaona kabisa kwamba hapa tunahitaji kuagiza ngano nje lakini mimi sikubaliani sana na hili suala la kuagiza ngano nje. Kwanza tunao hawa waagizaji wa ngano, tunaweza tukawatumia hawa hawa, tukawawezesha tukawapa maeneo, tukawapa extension services wakazalisha ngano, hata kama haitafikia hiyo tani 1,000,000 Watanzania sasa tubadili mitazamo yetu tuna chakula cha aina nyingi sana katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza mimi niwapongeze wale Watafiti ambao wamefanya utafiti na kuboresha viazi wakatengeneza viazi lishe wamevifanyia Biofortification sasa hivi unaweza ukapata keki nzuri sana kutokana na unga wa hivi viazi, ukapata maandazi na ukapata pia biscuit kutokana na hivi viazi, ninaomba tutumie pia mazao yetu. Tuna mazao ya aina nyingi sana tunayo mihogo, tunayo viazi mviringo, tunayo magimbi, tunao mchele tunapata pia hata mkate kutokana na mchele, vitumbua tunaweza tukatengeneza bagia kutokana na dengu tunalima dengu, tunaweza tukatengeneza bagia kutokana na kunde. Kwa hiyo mazao tunayo mengi sana ambayo tunaweza tukatumia, tuachane na huu mtazamo kwamba bila mkate bila chapati za ngano, bila maandazi huwezi ukanywa chai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna mazao kama korosho unaweza ukafanya mchanganyiko mzuri korosho, maboga pamoja na matunda ukapata breakfast yako nzuri sana, sitaki kuwarudisha labda kwamba tunafanya mambo ya kizamani lakini ndivyo vyakula ambavyo tunavyo na ni vyakula ambavyo vina lishe bora. Kwa mfano, maboga yanasaidia pia kwenye suala la kudhibiti diabetes, ni mazuri sana ukitumia ukaepukana na mkate au maandali ni mazao mazuri sana. Tunazo karanga pia kwa hiyo hata ndizi ni nzuri sana unaweza ukatumia kwenye breakfast uka-balance pamoja na karanga pamoja na matunda ukatengeneza mlo wako mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninaomba sana tutoe kipaumbele kwenye umwagiliaji wa mazao haya ili yaweze kupatikana kwa mwaka mzima, tunaweza pia hata tukawasaidia wakulima wetu wakapata kipato badala ya kupeleka fedha nyingi kununua ngano tani 1,000,000 wakulima wetu wadogo wanaweza wakapata kipato na wakatusaidia pia kupata lishe bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa hifadhi ya chakula naomba nizungumzie kidogo eneo hili muda ni mdogo, tuna matatizo ambayo yametokea wakati Fulani, watu wamepoteza maisha kutokana na sumukuvu na hii mara nyingine inatokana na hifadhi ambayo siyo nzuri ya nafaka au mazao ya karanga. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali kuna wasambazaji wa ile mifuko ambayo hairuhusu hewa kupita au unyevunyevu, tuhitimize sana hii mifuko isambae kwa wakulima wa mahindi ili waweze kuhifadhi nafaka. Naomba dakika moja, mifuko iweze kusambazwa kwa sababu hii inazuia sana sumukuvu na tunaweza tukapata chakula ambacho kipo safe zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna wale wabanguaji wadogo wa korosho wawezeshwe kupata vacuum sealer, Tanzania nzima ukitafuta vacuum sealer hazipo mpaka uagize nje na ukiagiza nje hizi zinatozwa VAT, mimi naomba VAT iondolewe kwenye vacuum sealer ili wabanguaji wadogo wabangue korosho na ziweze kuhifadhiwa vizuri kwa kutumia vacuum sealer.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesahau kuunga mkono hoja, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja hii ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kupewa tuzo ya kipekee kabisa kwa uendelezaji wa miundombinu, ambapo ninaamini kabisa kwamba miundombinu hii ni pamoja na ile ya sekta ya nishati, kwa hiyo nampongeza sana. Vilevile ninaipongeza Wizara hii kwa kazi nzuri ambayo inaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina masuala makubwa mawili katika eneo hili la nishati. Nianze kwa kuipongeza Wizara kwa kutenga shilingi bilioni 1.48 kwa ajili ya kusambaza gesi asilia majumbani katika viwanda na katika taasisi mbalimbali. Kwa kweli ni jambo moja la muhimu sana, na niseme kwamba usambazaji huu wa gesi asilia hasa kwa ajili ya kupikia utasaidia sana kupunguza matatizo ya uharibifu wa mazingira unaotokana na matumizi ya kuni na mkaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile itasaidia kupunguza matatizo ya kiafya kama yale ya maradhi ya mapafu na maradhi ya macho wenzetu katika nchi za wenzetu wameshafanya utafiti na kuonyesha kwamba matumizi hasa ya muda mrefu ya kuni na mkaa yana athari kubwa sana kiafya kwa akina mama na watoto na hasa kwa upande wa mapafu na upande wa macho, nasi wenyewe tumekuwa ni mashahidi, wakati mwingine Bibi zetu wanauawa kutokana kuonekana na macho mekundu wanakuwa na imani za kishirikina, wanawaua kwa sababu hizo lakini kumbe tatizo kubwa ni matumizi ya kuni na mkaa kwa muda mrefu, kwa hiyo ninaipongeza Serikali lakini niiombe iongeze fedha kwenye eneo hili kwa sababu kazi inayofanyika kwa kweli inakwenda taratibu sana tunaomba kasi iongezeke ili kusudi kuweza kuwanusuru hawa akina mama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongeze tena faida nyingine kubwa ambayo inatokana na matumizi ya gesi asili kwa kupikia ni ile ya kusaidia kupunguza matatizo ya lishe kwa katika kaya hasa kwa upande wa Watoto. Wenzetu wa FAO mwaka 2018 waliweka mkakati kuongeza upatikanaji wa nishati mbadala kama vile gesi na umeme kutasaidia sana kuimarisha lishe majumbani. Hii inatokana na kwamba akina mama wale watapata muda mwingi wa kuwahudumia watoto vilevile wanaweza wakapika vyakula vya aina mbalimbali. Kwa mfano unga wa dona kupika ugali unahitaji nishati ya uhakika lakini hata uji ambao tunashauri watoto watumie uji wa dona unahitaji muda mrefu, kwa hiyo niombe sana wizara iliangalie hili iongeze fedha ili kusudi wenzetu kule vijijini waweze kupata nishati ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la pili ni kuhusiana na zile uzalishaji wa megawatt 300 kule Mtwara, naomba niliambie Bunge lako Tukufu kwamba uwezo wa kituo cha kuzalisha umeme kule Mtwara ni megawatt 30 tu, lakini kwa sasa kuna mashine tatu ambazo ziko nje, kwa hiyo wanazalisha umeme megawatt 24, lakini matumizi ya umeme Mtwara la Lindi ni megawatt 22 kwa hiyo utaona kitu kinachobaki ni kidogo sana ni takribani megawatt Mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana hizi megawatt 300 ambazo wizara imesema kwamba itatoa kipaumbele kwenye huu mradi ifanya hivyo kweli. Kwa nini ninasema hivyo, nimeangalia kwenye randama nimeona hakuna bajeti katika miradi mingine ambayo Wizara imewekea kipaumbele kwenye mradi huu wa megawatt 300 wa Mtwara hakuna bajeti hata Shilingi Moja! Kwa hiyo niombe sana wakati wa majumuisho Mheshimiwa Waziri atuambie Wizara ina mpango gani kuhusiana na suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho ningependa Bunge lako Tukufu litambue ni kwamba, wakati wastani wa Kitaifa wa usambazaji wa umeme vijijini imezidi asilimia 80 kule Mtwara bado asilimia 51 ya vijiji havijafikiwa na umeme. Hata hivyo, bado tunayo mahitaji makubwa ya umeme ukiangalia sasa hivi tunahimiza sana viwanda vya uchakataji korosho, vipo viwanda 20 ambavyo havifanyi kazi hatujui tatizo ni nini, hata hivyo tunaendelea kuhimiza uanzishwaji wa viwanda vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo eneo la EPZ kule Mtwara maeneo ya bandari lile eneo wakienda wawekezaji pale tutahitaji umeme mwingi sana wa kutumia, kuna miradi mingine ya maji mikubwa kama vile miradi ya Makonde, mradi wa kutoa maji Mto Ruvuma, miradi hii itahitaji umeme mkubwa, sasa Wizara iniambie hizi megawatt Mbili sasa hivi tukikamilisha hiyo miradi itatosha kweli kuzalisha kutumika katika pampu kubwa za kuzalisha maji? Kwa kweli niseme Mtwara hatujatendewa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kiwanda cha Dangote pekee chenyewe kinahitaji zaidi ya megawatt 30 lakini wenyewe wanazalisha umeme wao, kwa maneno mengine tunataka kusema kwamba kwa umeme huu tulionao, kama tuta-neglect hizi megawatt 300 ina maana hakuna fursa za uwekezaji zaidi katika Mikoa ya Mtwara na Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Serikali ituangalie watu wa Mtwara na Lindi ituanzishie huu mradi wa uzalishaji umeme ili kusudi nasi tuweze kuwa na fursa za uwekezaji, nakushukuru sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia zawadi ya uhai pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote. Nichukue pia nafasi hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Nape Moses Nnauye kwa hotuba yake nzuri ambayo ameitoa, lakini vilevile kwa ujasiri na kazi kubwa ambayo ameifanya hadi kufikia hatma ya kufikisha Muswada huu Bungeni; hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuishukuru Kamati ya Bunge kwa ushirikiano wao na kwa kazi nzuri ambayo wameifanya ya kutengeneza vizuri Muswada huu. Vilevile niwashukuru watendaji wa Wizara kwa ushirikiano ambao wametupa hadi kufikia dakika hii tunayozungumzia Muswada huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumshukuru mume wangu mpenzi Lawrent Paul pamoja na familia yangu kwa kuniombea kila wakati. Kwa namna ya pekee kabisa naomba nichukue nafasi hii pia kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri sana na ya kujenga ambayo naamini kabisa baada ya hapa Muswada huu unakwenda kupita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Nina masuala machache sana, matatu tu ambayo nitayazungumzia. Suala la kwanza ni ushirikishwaji wa wadau. Nizungumzie ushirikishwaji wa wadau na hasa pale ambapo liliibuka suala kwamba wadau walihitaji wapate miezi miwili zaidi na kikubwa ambacho baadaye kimezungumziwa baada ya kuwa ufafanuzi wote wa kina umetolewa na Mheshimiwa Waziri na Kamati, lakini baadaye ikaibuka kwamba kulikuwa na hitaji la kufika mikoani ili kusudi wadau waweze kuongea na press clubs kule mikoani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nichukue nafasi hii kusema kwamba sisi Wizara tulikuwa tunajua kwamba tuna Muswada huu na tuligawana kazi na Mheshimiwa Waziri. Katika kazi zetu za Wizara tulikwenda mikoani na tulipokwenda mikoani moja ya kazi ambayo tuliifanya ni kukutana na press clubs.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwamba walitupa ushirikiano mzuri sana; walikuwa wazi kutoa changamoto zao wakajieleza vizuri, lakini kati ya hizo changamoto ambazo tuliziona ni za muhimu kuletwa na kuingizwa katika Muswada wa Huduma za Habari ni mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya kwanza ilikuwa ni masharti magumu ya kupata press cards na changamoto ya pili ilikuwa ni kutokuwa na bima katika kazi zao, lakini pia kulikuwa na uhitaji wa kuwekwa katika Mfuko wa Hifadhi za Jamii. Haya yote tumeyaingiza katika kifungu cha 12(a) kinachoeleza kwamba Bodi ya Ithibati itakuwa ikitoa ithibati lakini pia itakuwa ikitoa press cards. Nashukuru kwamba hata Waheshimiwa Wabunge akiwemo Msemaji wa Kambi ya Upinzani wameliunga mkono na wamelipongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la bima pia linaonekana katika kifungu cha 58; na hiki pia tumepongezwa kwamba ni jambo zuri ambalo limefanyika. Kwa hiyo, kimsingi suala la kuwashirikisha wadau na hasa pale ambapo tunatakiwa tuongeze muda mpaka mwezi wa Pili ili kusudi wale press clubs waweze kutoa mawazo yao, tayari tulikwishalifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la pili ambalo limejitokeza na nataka kulizungumzia ambapo inaonekana katika michango yetu tumekuwa tukichanganya kati ya leseni, ithibati pamoja na vitambulisho. Sasa naomba nitoe ufafanuzi tu kidogo hapa kwamba, masuala ya leseni; leseni zinatolewa kwa vyombo vya habari hasa machapisho na hili linaonekana kwa mujibu wa kifungu cha 8(1), ila masuala ya hawa waandishi wa habari wao hawapatiwi leseni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo, wasiogope kwamba watachukua mlolongo mrefu au watanyimwa uhuru wa kufanya kazi zao kwamba ni hadi wapate leseni, hao hawahusiki kabisa na leseni, wao wanachotakiwa kupata ni ithibati pamoja na vitambulisho. Kwa hiyo, wasiwe na wasiwasi kwamba kuna masuala ya leseni. Msuala ya leseni ni vyombo vya habari na kwa mujibu wa Sheria ya TCRA leseni ni kwa redio na televisheni, lakini kwa mujibu wa sheria hii inatolewa leseni kwa machapisho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kifungu cha 7(1)(b)(iv) ambacho pia imeonekana kama kuna tatizo. Wengi wamekuwa wakitetea kwamba kwa ule wajibu wa vyombo vya habari unaosema kwamba vyombo vya habari vitatangaza au kuchapisha habari au masuala ambayo ni muhimu kwa Taifa kwa kadri Serikali itakavyoelekeza. Kwa hiyo, imeonekana kwamba kwa sababu wao ni wafanyabiashara hawatahitajika kuagizwa na Serikali kutoa taarifa za masuala muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nachukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Mushashu kwa ufafanuzi mzuri ambao ameutoa jana, amelieleza vizuri sana jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee tu, kwa mfano, kuna nchi moja ya China, mwezi wa kumi kulitokea watabiri wa hali ya hewa, walitabiri kwamba kutatokea upepo mkali katika baadhi ya Majimbo kule China, lakini kwa kushirikisha vyombo vya habari waliweza kutangaza kwa wananchi kwamba upepo huu unatokea wapi na una speed gani. Vilevile, vyombo vya habari vikawatangazia wananchi wanunue chakula cha kutosha wiki nzima na wakaambiwa wakae ndani, wasitoke nje mpaka pale watakapotangaziwa kwamba hali imeshakuwa shwari na waliweza kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hilo, hayakuweza kutokea madhara makubwa kwa binadamu na badala yake yalitokea madhara madogo madogo ambapo ilikuwa magari yaliyokuwa yame-park nje miti ikawa imeangukia, lakini siyo kwa binadamu. Pia yalitokea madhara machache kwa wale ambao walikaidi na pengine wale wanaoendesha pikipiki, upepo ule kwa sababu ulikuwa ni mkali uliweza kuwazoa. Vinginevyo visingekuwa vyombo vya habari kushirikiana na Serikali, ina maana kwamba sasa hivi yangekuwepo madhara makubwa katika nchi ya China.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuunge mkono muswada huu kwa sababu una umuhimu mkubwa sana kwa wanahabari, kwa vyombo vya habari, lakini pia kwa kila mmoja wetu ambaye yuko hapa na kwa wananchi wote kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, narudia kusema tena, naunga mkono hoja, ahsanteni sana.