Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Angelina Adam Malembeka (24 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Ninaitwa Angelina Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Kaskazini, Unguja.
Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufika hapa. Nashukuru Chama changu cha Mapinduzi na Jumuiya zake zote tatu kwa kazi nzuri iliyoifanya ya kufanya kampeni nchi nzima na kutuwezesha Wabunge wa Viti Maalum kuingia humu ndani, sambamba na Wabunge wa CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naunga mkono kwa nguvu zangu zote hotuba ya Mheshimiwa Rais Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wamechangia mengi kuhusiana na michezo, wanahabari, elimu, afya, maji, reli, umeme, kilimo uvuvi, rushwa, barabara, utawala bora, biashara, ukusanyaji wa mapato na mengineyo yote nayaunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wangu katika hotuba ya Mheshimiwa Rais, napenda kuchangia ukurasa wa 35 paragraph ya pili na ukurasa wa 36 paragraph ya pili; kwa ridhaa yako naomba niyarudie maneno yale. Ukurasa wa 35, paragraph ya pili inasema; “Mheshimiwa Spika, tunaitwa Waheshimiwa kwa heshima ya dhamana tuliyopewa na Bunge hili Tukufu, tutunze heshima hiyo ili tuzidi kuheshimiwa.” Mwisho wa kunukuu.
Ukurasa wa 36 unasema; “Mheshimiwa Spika, nimejitahidi kuzungumza kwa uchache, lakini napenda kukushukuru sana tena, Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa viongozi wote, tuliokaribishwa kuingia katika ukumbi huu na kuhudhuria yaliyojitokeza na mmeona kuna kazi kubwa, kwa sababu bado kuna watoto wengi, mwendelee kuwavumilia na kuwafundisha na Watanzania wamewaona.” Mwisho wa kunukuu na baada ya hapo kilifuata kicheko na makofi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ni maneno makali ambayo Mheshimiwa Rais ameongea kwa unyenyekevu mkubwa. Yale maneno ukiyaangalia kwa haraka unaona yanachekesha, lakini maneno hayo ni makali. Humu ndani hakuna watoto! Kuna watu wazima, Waheshimiwa Wabunge, wenye umri mkubwa na wenye busara; lakini kutokana na sababu za wachache humu ndani watu wote tunaonekana watoto. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, humu ndani tumeshindwa kuonesha nidhamu kati ya Wabunge na Wabunge, tumeshindwa kuonesha nidhamu baina ya viongozi wetu wa nchi, tumeshindwa kuonesha nidhamu kwa viongozi wetu wa vyama, tumeshindwa kuonesha nidhamu baina ya Wabunge na viongozi wetu wa Bunge tuliowachagua, lakini pia tumeshindwa kuonesha nidhamu kwa wananchi waliotuchagua.
Mheshimiwa Naibu Spika, humu ndani wanasema siyo shwari. Mimi nasema humu ndani ni shwari, isipokuwa siyo shwari kwa wale wa upinzani. Wamekuwa wakilalamika kwamba Chama cha Mapinduzi tunakula pesa, tunamaliza hela ya Serikali, tunamaliza hela ya umma.
Mheshimiwa Naibu Spika, wewe utakuwa shahidi, wanakuja hapa, wanasaini, wanachukua hela ya wananchi, wanaondoka. Hivi ni nani alienda kuomba kura akisema naomba mnichague nikamzomee Rais? Ni nani alienda kuomba kura akasema, nipe kura yako niende nikamzomee Spika? Ni nani aliyeomba kura akasema, ninaomba kura yako niende nikamzomee Mwanasheria Mkuu wa Serikali? Ni nani aliyeomba kura akasema ninaomba kura yako ili niende nikawazomee Wabunge? Ni nani aliomba kura akasema naomba nichague ili nikisaini posho nitoke? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunalidhalilisha Bunge! Tunakula pesa za wananchi bila sababu. Kama kweli wana uchungu wakae ndani ya ukumbi huu waongee, wachangie hoja, tuzijibu, tushindane kwa hoja, siyo kwa kuzomeana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme, wamekaa wanalalamika, Zanzibar siyo shwari. Mimi natoka Zanzibar, Kitope, Kichungwani, Mkoa wa Kaskazini Unguja, Jimbo la Mahonda. Sijatemewa mate, sijapigwa makofi na niko salama, isipokuwa wao kwao siyo shwari, ndiyo maana kutwa wanazomea.
Mheshimiwa Naibu Spika, humu ndani kuna watu wana heshima zao, watu wakubwa sana; tuna watoto wa Marais ambao wako humu ndani, wameingia kihalali kama Wabunge, hawezi kukubali baba zao wanatukanwa tunawaangalia. Kuna watu humu sisi ni shemeji zetu, wajomba zetu, watoto wetu, wakwe zetu, wanatukana humu ndani tunawaangalia. Uvumilivu una mwisho wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, siku zote huwa wanasema nyoka wa kijani haumi, mimi ninakuhakikishia siku akiuma hana dawa! (Makofi/Kicheko)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa Mzungumzaji)
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie, kama mtu anasema hataki… (Kicheko/Makofi/Kelele)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hotuba ya Rais. (Kicheko/Makofi/Vigelegele)
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, naomba kufanya mabadiliko ya usajili wa kijiji cha Sibwesa kwenye karatasi yangu niliyochangia kwa maandishi badala ya kusajiliwa mwaka 1967 sahihi ni kuwa Kijiji cha Sibwesa kilisajiliwa mwaka 1975 na hati ya usajili wa kijiji hicho kusainiwa tarehe 20/5/1976 hivyo mgogoro huu una zaidi ya miaka 31.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri, nawapongeza watendaji wote wa Wizara hii naunga mkono hoja. Pia nampongeza Waziri na Naibu Waziri wake kwa jinsi wanavyoweza kushuka na kupokea ushauri na maoni wanayopewa na wadau wa maliasili na utalii mfano kundi la uhamasishaji wa utalii wa ndani uitwao Utalii 255.

Mheshimiwa Spika, Waziri na Naibu Waziri kwa wakati mbalimbali walipata fursa ya kuzungumza na wadau hao.

Katika suala zima la uwindaji, nashauri muda wa kuwinda unapofika taarifa itolewe kwa uwazi kupitia vyombo mbalimbali vya habari. Taarifa hiyo ieleze muda wa kuwinda, gharama zinazotakiwa kulipwa, aina ya silaha zinazoruhusiwa kutumika na kadhalika. Kwa sasa taarifa hizo hazipo wazi kwa wananchi ambao wangependa kupata kitoweo chenye ladha tofauti kinachopatikana nchini.

Mheshimiwa Spika, katika nchi jirani ya Kenya kuna ukumbi wa burudani mjini Nairobi unajulikana kwa jina la Carnival, kuna aina tofauti za nyama choma kutoka mbugani mfano nyati, nyumbu, swala, mbuni na kadhalika. Huku kwetu jambo hilo halipo hivyo Tanzania tunafanya utalii na kuwatunza lakini wenzetu wanatafuna!

Mheshimiwa Spika, suala la maeneo ya hifadhi na changamoto zake, kazi za ulinzi katika maeneo hayo inafanyika vizuri sana. Naomba ubinadamu ufanyike, kuna tofauti kubwa ya majangili na wananchi wanaoingia katika hifadhi kupata dawa, kupata miti ya kuni au kutengeneza mipini ya majembe na mashoka. Ukweli wananchi hao wanapokutwa huko adhabu wanayoipata ni kubwa kuliko kosa walilolifanya. Wengine wamepata vilema hata kupoteza maisha. Naomba elimu itolewe zaidi kwa wananchi ili kuwaepushia na adhabu hizo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu uanzishwaji wa vituo vya utalii wa ndani katika mikoa mbalimbali nchini, vituo hivyo vitasaidia kuleta hamasa na ushindani baina ya Mkoa na Mkoa, utasaidia wananchi kusafiri umbali mdogo ili kufikia vituo. Kama malipo yatawekwa kidogo itasaidia wananchi wengi kutembea na kuingiza mapato kwa Serikali.

Mheshimiwa Spika, katika uhamasishaji wa utalii wa ndani, kuwe na utaratibu wa kuwazoesha watoto na wanafunzi kutembelea vivutio mbalimbali na kuelezewa umuhimu wa kutunza tunu zetu na kuwa wazalendo, watoto hao na wanafunzi wataendeleza tabia nzuri ambayo itasaidia kuondoa au kupunguza mambo ya ujangili na uvunjaji wa sheria na kuisadia katika kulinda tunu zenu.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Wizara hii kwa kuitangaza nchi yetu ndani na nje ya nchi. Naipongeza kwa kuingizia Serikali mapato kupitia vivutio mbalimbali, nampongeza Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante.
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nichukue nafasi hii kwanza kutamka rasmi naunga mkono mapendekezo ya Mpango. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchangiaji wangu utajikita katika suala zima la viwanda, lakini pia nitazungumzia masuala ya Zanzibar kama wengine walivyozungumza japo tunaandaa Mpango Kazi. Napenda utambue kwamba kitambulisho changu cha Uzanzibar ni Na.010242768 ambacho ni halali na kitambulisho changu cha Tanzania ni Na.196650102-12114-0001-17. Nimeona nijitambulishe nafasi hiyo ya Uzanzibari kwa sababu kuna watu Zanzibar wanaijua kwa ramani lakini wanaisema kama vile wanakaa kule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Zanzibar tuliiachia Tume ya Taifa ya Uchaguzi Zanzibar ambayo imetoa maelekezo na mpambano ni tarehe 20 Machi, 2016. Huwezi ukakaa unasema wewe unaendekeza demokrasia, unaijua na unataka haki itendeke wakati unawaaambia wananchi wako wasiende kupiga kura. Demokrasia ya kweli inachagua viongozi wanaowataka wao siyo kwa kiongozi mmoja kutamka watu wangu msipige kura, hiyo demokrasia ya wapi? (Makofi)
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuhakikishia Zanzibar ni shwari na salama atakaye aje. Zanzibar ingekuwa siyo shwari Wabunge tusingekuwa hapa. Wabunge wote tungekuwa tumeshaenda Zanzibar kwa ajili ya hekaheka ya Zanzibar lakini Wabunge kutoka Zanzibar tuko hapa hii inaashiria jinsi gani Zanzibar iko shwari. (Makofi)
(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walikuwa
wakiongea bila mpangilio)
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kukumbusha, humu ndani hakuna Amiri Jeshi Mkuu anayeweza kutangaza hali ya hatari. Nakumbuka tarehe 29 Oktoba, 1978, Nduli Iddi Amini alivyoingia Tanzania, Amiri Jeshi Mkuu ndiye alitangaza kwamba tuna hali ya hatari nchi yetu iko kwenye vita. Sasa humu ndani ni nani aliyekuwa Amiri Jeshi Mkuu anayetangaza Zanzibar si shwari? (Makofi/Kicheko)
(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walikuwa
wakiongea bila mpangilio)
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa siku zijazo, kwa kuwa Wabunge tunatoka kwenye kampeni tukija hapa labda kidogo akili zina-change itabidi tupimwe kwanza akili ndiyo tuingie Bungeni. (Makofi/Kicheko)
(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walikuwa
wakiongea bila mpangilio)
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu mpaka sasa hivi wanaongea wanafikiri wako kwenye kampeni, wamesahau kwamba kampeni zimekwisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie Mpango na kama nilivyosema nauunga mkono. Tunavyo viwanda ambavyo vinahitaji kufufuliwa, naomba viwanda vile vifufuliwe vikiwepo vya korosho na vya nguo. Sambamba na hilo naunga mkono pia utaratibu wa kujenga viwanda vipya, naomba vijengwe katika maeneo husika ambapo malighafi inapatikana. Isije ikawa kama tulivyofanya Kiwanda cha Almasi kinajengwa Iringa wakati almasi haipatikani Iringa. Naomba tuangalie kipaumbele cha namna hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo naomba vijana wetu wawezeshwe katika kupata elimu ya utaalamu huo ili tusije tukajaza wataalamu kutoka nje na vijana wetu wakakosa ajira. Katika ajira hizo, naomba vijana waangaliwe zaidi siyo kwamba hatutaki uzoefu wa wazee, tunaomba ule uzoefu uende pamoja na uzeefu muda ukifika wastaafu ili vijana wapate nafasi. Kumekuwa na tabia baadhi ya wazee ambao wako kwenye nafasi wanapoanzisha mradi wanaanza kubadilisha majina, anakuwa Project Manager inapokuja kuanza kazi wanatengeneza CV zinazolingana na wao walivyo ili vijana wasipate ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba hali hii ibadilike vijana wapewe ajira na experience wataipata wakiwa kazini, wanayo nafasi ya kujiendeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba wafanyakazi walipwe mishahara mizuri ili kuondoa migogoro kwenye viwanda hivyo. Kwa sababu kama kutakuwa na migogoro viwanda vitafungwa vitashindwa kuzalishwa na majipu yatazidi kuonekana. Katika hili nikukumbushe majipu mengi makubwa huwa yanatoa na alama ya sehemu gani ukamue ili kiini kiweze kutoka. Upande wa pili unaong‟ang‟ania CCM tuna majipu kule kuna matambazi, yale majipu makubwa ambayo hayaoneshi mdomo uko wapi? Mimi nikuhakikishie majipu ya namna ile lazima yatumbuliwe na mikasi. Majipu makubwa makubwa kama yale ambayo yanaitwa matambazi mengi yako upande wa pili japo hawataki kuyasema. (Makofi/Kicheko)
(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walikuwa wakiongea bila mpangilio)
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine napenda kuongelea kuhusu sekta binafsi. Naomba sekta binafsi zipewe ushirikiano wa kutosha kwa kuondoa urasimu na ukiritimba ili waweze kufanyiwa maamuzi ya haraka ili vijana wetu wapate ajira na tupate maendeleo ya haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, naomba niseme naunga mkono wale wote waliochangia kuhusu kuboresha miundombinu ya umeme, bandari, barabara, maji, reli na mawasiliano ili tuweze kufikia malengo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na nasisitiza, Zanzibar ni shwari atakaye na aje. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nami naungana na wenzangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri wote na Manaibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya. Kwanza niseme kwa moyo wangu wa dhati naipongeza Hotuba ya Waziri Mkuu kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika cchango wangu nitaanza na suala la ukusanyaji wa mapato. Kwa kuwa ukusanyaji wa mapato ni suala la Muungano, napenda pia tuiangalie bandari yetu ndogo ya Mkokotoni. Bandari ile huwa inachukua mizigo ya kwenda Tanga, Mombasa, Dar es Salaam na maeneo mengine kimya kimya. Sasa naona ni vizuri tuiangalie bandari yetu ya Mkokotoni tuweze kuiboresha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, katika bandari yetu ya Mkokotoni ni vizuri pia tukaandaa kivuko ili tuweze kuwasaidia wananchi wa Jimbo la Tumbatu. Wananchi wa Jimbo la Tumbatu kwanza hakuna gari hata moja, siyo kwamba Serikali imeshindwa kutokana na miundombinu iliyokuwa kule, hakuna.
Sasa ni vizuri basi tuwasaidie kuwe na kivuko cha uhakika kupitia ukusanyaji wa mapato utakaotokana katika bandari ile. Kabla sijaendelea kuchangia, napenda nikumbushe; wakati nachangia hotuba ya Mheshimiwa Rais, nilishasema kwamba inawezekana na itawezekana ifike wakati Waheshimiwa Wabunge tuanze kupimwa akili kabla ya kuingia Bungeni. (Makofi, Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kanuni zipo, watu wana akili zao timamu, lakini wao wamegoma wenyewe kuongea kwa idadi yao, halafu mwenzao akiongea, wanamtilia fujo.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina akili zangu timamu nimetumwa na wanawake wa Mkoa wa Kaskazini Unguja kuja kuwasemea.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Siwezi kuja hapa nikasaini posho ya mwezi ya kikao…
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: …halafu nikakaa kimya.
MBUNGE FULANI: Taarifa!
MWENYEKITI: Mheshimiwa Malembeka, naomba ukae, kuna taarifa!
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: …halafu nikakaa kimya.
MBUNGE FULANI: Taarifa!
MWENYEKITI: Mheshimiwa Malembeka, naomba ukae, kuna taarifa!
MWENYEKITI: Mheshimiwa Malembeka, endelea.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa mwenyekiti, ahsante. Kwanza taarifa yake naikataa kwa sababu hajitambui.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukusanyaji wa mapato ni wa Muungano, ndiyo maana na Mawaziri wa Fedha kule Zanzibar na hapa wapo. Sasa kwa kuwa yeye hajui ukusanyaji wa mapato ni suala la Muungano, naomba akajifunze na aende kule Baraza la Wawakilishi Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu na ninaendelea. La pili nataka nikuhakikishie, kwa umri niliokua nao, sijawahi kumwambia housegirl wangu aache kazi kwa ajili ya kuangalia TV kwa sababu najua madhara yake. Mboga zitaungua, kazi zitakuwa hazifanyiki na ana muda maalum kwa kufanya ile kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani mtu umetumwa na Jimbo lako, unkuja hapa unashindwa kuchania eti kwa sababu ya TV. Mbona housegirls wenu mnawakataza kuangalia TV? Mna matatizo gani? Huko kwenye TV kwenyewe kuna mambo yanafanyika ambayo hayaruhusiwi kuonekana hadharani. Watu wanabadilkishana Tai, watu wanapaka poda, watu wanabadilishana vipindi, hatuonyeshwi moja kwa moja. Vinazuiwa! Kwa nini Bunge mnaling’ang’ania hivyo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika ukurasa wa 12, suala la viwanda. Naipongeza Serikali yangu sikivu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri inayoifanya. Ni mikakati iliyojipanga kwa ajili ya kuboresha na kuanzisha viwanda kwa ajili ya manufaa ya wananchi wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba katika mkakati ule, tuangalie upya wawekezaji wetu kutokana na kwamba kuna baadhi ya wawekezaji ambao wanapenda sana kuwanyanyasa wananchi wetu wakiwepo vijana wanaofanya kazi katika maeneo yale. Ninafurahia viwanda viwepo na vigawanye katika Kanda mbalimbali ili kila Mkoa uweze kufaidika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi pia ni mdau wa Jimbo la Ukonga, nina nyumba yangu kule na nimekuwa Diwani kwa miaka kumi. Kwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Ukonga Chama chake kimemkataza kusema, naomba niseme haya kwa niaba ya Mbunge wa Ukonga ambaye kanyamaza. (Makofi/Vigelegele/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Ukonga nataka nizungumzie Barabara. Kuna barabara iliyoanzishwa miaka ya nyuma, naomba Serikali imalizie. Ni barabara ya Chanika - Kitanga mpaka Masaki, kuna barabara ya Chanika - Homboza mpaka Masaki, kuna barabara ya Mvuti kuelekea Dondwe, barabara ya Pugu – Majoe - Mbondole, barabara ya Mbondole -Msongola mpaka Mbande, barabara ambayo inatoka Banana – Kitunda - Kivule hadi Msongola.
Barabara hizo ziliweza kufanyakazi na wananchi wana shida na barabara zile na Mbunge wao amekatazwa kusema; ninaomba kama Mbunge wa Viti Maalum mwenye hisia na Jimbo la Ukonga, nalisemea Jimbo hilo. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado nikiwa na uwakilishi wa wananchi napenda niingie katika ukurasa wa 54 Sekta ya Afya. Katika Jimbo la Ukonga, bado tuna Hospitali ya Kivule. Naishukuru Serikali hii imetenga fedha ya kuongeza kwa ajili ya kukamilisha hospitali ya Kivule.
Naomba Serikali isaidie pia kwa ajili ya Zahanati.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: …ilianzishwa kwa nguvu kubwa ya Mheshimiwa Jerry Silaa akiwa Mstahiki Meya kwa ridhaa yake. Naomba Serikali i-support tukamilishe.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Malembeka, naomba ukae kuna taarifa!
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Zahanati ya Mbondolwe, Luhanga, Lubakaya na Yongwe, ziweze kufanya kazi katika Jimbo la Ukonga. Nataka nizungumzie kuhusu; eeh!
MWENYEKITI: Mheshimiwa Malembeka, naomba ukae, kuna taarifa. Haya Mtoa taarifa
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na ninaomba muda wangu uendelee kulindwa.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza taarifa naikataa. Nimekuwa Diwani miaka kumi nikikaa ndani ya Jimbo la Ukonga, sikumjua. Haya ninayozungumza nina uhakikanayo, niliyapanga nikiwa Mwenyekiti wa Huduma za Jamii Manispaa ya Ilala.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kuhusiana na vita dhidi ya rushwa na ufisadi. Napongeza kwa dhati juhudi zinazofanywa na Mheshimiwa Rais za kupasua majipu na ninaomba majipu haya yasiishie ndani ya wananchi wa huku, twende kwenye Vyama.
Hata kama mtu akibadilisha shati; akivua shati la kijani akivaa leupe, tumfuate huko huko, tukamtumbue. Kwa sababu wengine wamehama; wametoka huku wameenda upande wa pili. Tuwafuate tukawatumbue majipu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kuhusiana na suala la vijana kwa upande wa bodaboda. Nafurahi kwamba Serikali hii imewatambua bodaboda, naomba waendelee kupewa mafunzo, waelekezwe waweze kukata Bima ya Afya, lakini pia naomba Serikali hii iandae utaratibu kuona jinsi gani ya kuagiza vifaa vya bandia kwa sababu sasa hivi tumepata walemavu wengi sana kutokana na suala la bodaboda. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niingie ukurasa wa 21 kwa ajili ya suala zima la walemavu. Naishukuru Serikali yangu Tukufu ambayo ni sikivu, imeweza kutenga mambo maalumu kwa ajili ya walemavu. Ninaomba tuendelee kuwasaidia kupata miradi na kuwapa elimu, tuwasaidie kuwapangia maeneo ya kufanya biashara zao. Lakini pia tuangalie utaratibu wa kuwapunguzia masharti ili waweze kupata mikopo nafuu na kuendesha biashara zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe masikitiko yangu; nasikitika sana kuona baadhi ya walemavu viungo vyao wanafanya kama vile mradi au kichekesho. Kile kitendo, binafsi mimi kinaniuma, kinaniudhi. Ninafahamu kabisa ulemavu siyo kushindwa, lakini bado wapo baadhi ya walemavu wanakubali kutumika kama kichekesho kwa ajili ya shughuli nyingine. Mimi hiyo tabia kwa kweli siipendi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niongelee zaidi pia kuhusiana na suala la maslahi ya Watumishi. Siku zote niseme kwamba kazi nzuri inavyoenda na kazi yoyote utamu wake fedha. Hatuwezi tukakaa kila siku tunataja section mbili tu; Walimu, Madaktari! Naomba nisemee sekta nyingine zote zilizobaki kwamba maslahi yao yaboreshwe ili waweze kufanya kazi vizuri na kwenda sambamba na kasi ya Hapa Kazi Tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka pia nizungumzie katika suala zima la…
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Malembeka, inatosha naomba ukae muda umemalizika.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Eeeh! Muda umeisha!
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa muda umeisha namalizia kwa kusema kwamba nyoka wa kijani haumi, siku akiuma hana dawa. Naunga mkono hoja!
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuingia katika kikao hiki cha bajeti kwa awamu hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naunga mkono hoja za Mawaziri wote wawili kwa asilimia mia moja. Nachukua pia nafasi hii kuwapongeza Mawaziri wote wawili pamoja na Naibu na team zao zote wanazofanya nazo kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, michango yangu itakuwa michache na nitajaribu kuitoa kwa ufupi sana. Nianzie na mpango wa MKURABITA. Nachukua nafasi hii kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri sana wanayoifanya. Nimepita miradi mbalimbali ya MKURABITA na nimeona jinsi gani wananchi walivyohamasika na jinsi walivyokubaliana na shughuli ya MKURABITA na hivyo kuweza
kumiliki ardhi na kuwa na hati ambazo zinawezesha kupata mikopo katika taasisi za fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali yangu kwa kuwa wananchi wameridhia ni vyema kabisa kwamba kwa sasa hivi shughuli hii iende moja kwa moja nchi nzima kwa kuangalia Majimbo ili kila Jimbo angalau tuwe na mfano mmojawapo wa kufanyia hii kazi. Nimeona
akinamama jinsi walivyopata hati za kumiliki ardhi pamoja na vijana, kwa hiyo, nashukuru na naiomba iendelee kufanya kazi vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la TASAF, nimepita katika miradi mbalimbali nimeangalia, nimeona TASAF jinsi ilivyofanya kazi vizuri na kuwezesha watu wenye kipato kidogo kuweza kujenga nyumba, kupeleka watoto wao shule na kuwanunulia uniform, lakini pia na kubuni miradi mbalimbali ambayo imewawezesha kuongeza kipato.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba, kwa wale Watendaji wachache ambao hawakuwa wema, wakaamua kuvuruga utaratibu huu, nafahamu kwamba wamechukuliwa hatua, lakini ni vyema Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa, atuambie wale watendaji ambao kwa
makusudi wameamua kuvuruga utaratibu huu wamechukuliwa hatua gani? Badala ya kuwalazimisha wananchi walipe pesa ambazo hawakuziomba. Wale waliowajazia ndio walikuwa na matatizo. Kwa hiyo, tuwanusuru wale ambao wanalipishwa fedha ambazo hawana uwezo wa kulipa, tuwashughulikie wale waliowaandikisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika Mfuko wa Rais wa Uwezeshaji. Mfuko huu umefanya kazi vizuri sana, nampongeza Mheshimiwa Waziri na team yake yote, kwa sababu vikundi vya vijana ambavyo vimewezeshwa na Mfuko huu vimefanya kazi vizuri, lakini fedha zile zinazotolewa
zimekuwa chache. Ni vizuri tuangalie uwezekano wa kuwaongezea ili waweze kufanya kazi na kujiajiri wenyewe. Kwa sababu katika vikundi nilivyopitia, nimekuja kugundua kwamba siyo wote ambao elimu yao ni ndogo, wapo ambao wana elimu kubwa, wamejiunga na
wamewachukua wenye elimu ndogo na kufanya mradi wa pamoja hivyo kuweza kuajiriana wenyewe kwa wenyewe. Kwa hiyo, nawapongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia suala la TAKUKURU. TAKUKURU imefanya kazi nzuri, japo watu wanabeza. Kwa sasa hivi suala la rushwa limepungua, kwa kiasi kikubwa na kama Mheshimiwa Waziri alivyoelezea, wameweza kuokoa mamilioni kadhaa kutokana na mchakato uliofanywa katika kukagua na kutenda kazi zao. Ninachoshauri, fedha zile mmeeleza zimeenda Serikalini, lakini hatujaambiwa zimeenda kufanya nini? Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie fedha hizo walizookoa zimeenda kufanya nini? Kwa sababu bado tuna matatizo kwa wananchi, fedha hizo zinaweza zikatumika kwa ajili ya kazi nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kidogo suala la Usalama wa Taifa. Suala la Usalama wa Taifa ni suala nyeti na kama ni suala nyeti, naona kuna watu wanalifanyia uzembe uzembe tu. Mtu anaamka asubuhi, anatuma message, nimetekwa nyara. Hivi kutekwa nyara mchezo!
Mnatania suala la kutekwa nyara! Yaani mtu anatuma message, “nabadilisha nguo, naenda Polisi, nimetekwa nyara. Huko kutekwa nyara, mbona mnaifanyia utani taasisi hii!
Mheshimiwa Naibu Spika, mtu ananyanyuka, anasema Wabunge 11 watatekwa nyara; yeye alikaa nao vikao akawajua hao Wabunge 11! Naomba Usalama wa Taifa kwanza wawanyanyue wale waliosema kuna Wabunge 11 humu watatekwa nyara, watutajie ni akina nani? Walikaa
wapi? Wanatekwa nyara kwa kosa gani? Kwa sababu Usalama wa Taifa, mimi nategemea mpaka tumekaa hapa, ni kwamba wako kazini na wanafanya kazi vizuri. Ni vizuri basi wakaongezewa fedha katika idara yao, wapate mbinu mpya za kufanya kazi, waongezewe vifaa tuweze kupata usalama zaidi. Mtu kutwa, anaamka asubuhi anatuma message kwa rafiki yake, “nimetekwa nyara.” Hebu waulizeni waliotekwa
nyara, hiyo simu unaipata wapi ya kutuma hiyo message? Kutekwa nyara mchezo! Hebu waulizeni wanaotekwa nyara, watakwambieni ukweli.
Mheshimiwa Naibu Spika, huu mchezo wale wanaojifanya usalama fake, naomba Mheshimiwa Waziri unayehusika washughulikie. Kwa sababu sasa hivi mtu akishakata panki lake, akavaa kaunda suti yake, anatoa kitambulisho; mimi Usalama wa Taifa. Usalama wa Taifa
mchezo! Mtu amejizungusha zungusha tu huko, anawatisha watu mtaani, anasema Usalama wa Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wale ambao wanajifanya Usalama wa Taifa na kuwahenyesha watu mtaani, washughulikiwe. Wale wanaojifanya Usalama wa Taifa, kutoa data za uongo, washughulikiwe; sambamba na data za uongo za kwenye mitandao. Tumechoka! Nchi iko juu juu; watu tuko juu juu tunahangaika! Usalama wa Taifa wapo, mnawanyanyapaa; hebu fanyeni kweli; na tuanzie humu humu ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, mtu anasema hapa ushahidi ninao, usalama wa Taifa upo, hamjamchukua mpaka leo kuja kukwambieni Mbunge gani aliyetekwa nyara; mnamwacha tu, kwa nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie suala la utawala bora nikienda sambamba na maadili ya viongozi. Tumekaa muda mrefu tukizungumzia Ma-DC, Ma-RC tunajisahau sisi humu ndani. Maadili tuanze nayo sisi wenyewe na uongozi tuanze nao sisi wenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, kukaa humu ndani miaka 30 au miaka mitano; kama toka mwanzo wamekuja na mpango wako wa kutukana, utafikiria utaratibu wa huku ni wa kutukana. Naomba semina hizi zianze pia na kwa Wabunge ili tuweze kuwasimamia wenzetu. Kama semina
hizi watu watapata, kila mtu atajua wajibu wake ni nini, mamlaka yake na madaraka yake yanaishia wapi? Hatutazozana na DC, RC na wala wao hawatazozana na Wabunge. Isipokuwa kwa sababu semina hizi hazipo, ndiyo maana kila mtu anajiona yeye kubwa kuliko.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao Ma-RC, Ma- DC wazuri sana, wanafanya kazi vizuri sana; lakini wale baadhi ambao wanakosea ni sawasawa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walioko humu wanaofanya kusudi. Kuna wakati nilisema tupimwe akili, watu wakacheka, lakini
tunakoelekea itafika wakati watu watapimwa akili humu ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu yanayofanyika huku unajiuliza kweli huyu kiongozi, wanafikiria kujaza zile form za maadili ndiyo maana yake umemaliza maadili ya viongozi kumbe ni pamoja na matendo tunayoyafanya.
Taarifa....
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba unitunzie muda wangu. Pili nataka kumwambia anayeongea, hiyo taarifa yake siipokei. Kwanza naona kazuka tu! Kwa sababu suala la Usalama wa Taifa, imeitwa Taifa; haijaambiwa wa chama wala wa idara fulani. Ina maana hapa tulipo wenyewe wapo na wanafanya hiyo mambo yake halafu asijadiliwe, ndiyo maana mnaitwa mnahojiwa. Ingekuwa hivi hivi, humu ndani kusingekuwa salama. Iko siku humu ndani mtu angetoka vichwa vingebaki humu; lakini kwa sababu watu wapo na wanatulinda, ndiyo maana mnaona amani ipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme kwamba, suala la Usalama wa Taifa wasilichukulie mchezo, mchezo. Watu wana-support tu; wakisikia fulani katekwa nyara, hata kwa message wanakubali. Ninachosema ni kwamba, tunaomba amani iwepo na ninaendelea kusisitiza wale Wabunge waliosema wanawajua 11 wapo, watutaje; inawezekana labda na mimi nimo, nijue ni jinsi gani ninavyojilinda. Hawawezi kusema halafu wakaachwa na wamesema wanao ushahidi. Mmeona!
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kabisa, asubuhi tunaingia hapa tunaomba dua, tunawaombea na viongozi wetu na Rais tunamwombea; baada ya dakika kumi, wanamtukana halafu wanasema hashauriki. Sasa hata ungekuwa wewe, huyo mtu anakudharau, anakutukana,
unamwita akushauri nini? Kwa sababu kinachotakiwa hapa Wabunge tumepewa nafasi ya kuishauri Serikali na kuisimamia. Muda tunaopewa kuishauri Serikali na kuisemea, hatufanyi hivyo, tunaikashifu na kuitukana, halafu mkihojiwa mnasema kuna kanuni. Kuna haja ya kuja kubadilisha hizi kanuni ili watu tuheshimiane vizuri humu ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema kwamba kama suala la kuheshimiana, tunavyoapa hapa, tunajaza form, tuendelee kuheshimiana na tumheshimu kila mtu kwa nafasi yake. Mheshimiwa Rais sio mtu wa kumtukana; asubuhi huwezi ukamwombea dua, mchana unamtukana, wajirekebishe.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilisema siku moja kwamba nyoka wa kijani huwa haumi, siku akiuma hana dawa. Sasa yule nyoka kaanza kufanya kazi; wakiitwa kuhojiwa wanasema wametekwa nyara. Hatuteki nyara mtu! Mnatakiwa mkatoe maelezo kwa nini mnatukana? Ujiulize,
kwa nini kila siku unahojiwa wewe? Jiulize, kwa nini kila siku unaitwa wewe Polisi? Ukishapata jibu utanyamaza.
Mheshimiwa Naibu Spika, namalizia kwa kusema kwamba naungana na wenzangu wote wanaotetea Madiwani posho zao ziongezeke.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika bajeti hii. Kwanza nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri wa Fedha na timu yake yote. Sambamba hilo, nitoe pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi nzuri anayoifanya hasa ikionyesha wazi kwamba ana nia njema ya kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa manufaa ya Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Pamoja nakuunga mkono hoja, nataka nimtoe wasiwasi Waziri wa Fedha na timu yake kwamba ndugu zangu tumewazoea, watasema pale, baada ya dakika mbili watgeuka watakuja huku huku, watapita kwa Mawaziri, watawanong’oneza, Jimboni kwangu hakuna maji, Jimboni kwangu nataka shule, Jimboni nataka barabara, wanakuja huku huku. Mimi nakaa hapa hapa wanawaona. Mara wameenda kwa Waziri wa Fedha, mara Waziri wa Ardhi, mara Waziri wa Maji, mara wa TAMISEMI, mimi niko hapa hapa nawatazama; lakini wakipewa fursa ya kuchangia, wao ni hapana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapana hizi ifike sehemu na sisi tujirekebishe, tusiwe tunapenda mno anaposema hapana tunamlazimisha kumpa kitu. Hii ni bajeti ya nne katika Awamu hii ya Tano. Mara ya kwanza tumesema hapana, tumefanya kazi nchi nzima bila ubaguzi Majimbo yote, kazi imeonekana. Hakuna Jimbo lolote ambalo litasema halina shule ya msingi, halina shule ya sekondari, halina kituo cha afya, hana mwalimu, hana nesi, hana mtendaji, hana mkurugenzi. Hawa wote bajeti yao inapita hapa na tunachangia. Juu ya hilo …..

TAARIFA

MHE. YOSEPHER F. KOMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Angelina Malembeka, kuna taarifa Mheshimiwa Yosepher Komba.

MHE. YOSEPHER F. KOMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba nimpe taarifa mama yangu mzungumzaji kwamba maendeleo ambayo yanatokana na bajeti ya humu ndani siyo kwamba ni hisani ya Wabunge na hawapewi Wabunge, bali wanapewa wananchi kutokana na kodi zao. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Angelina Malembeka endelea na mchango wako.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee ila nikukumbushe, kuna wakati tunaingia Bungeni, niliomba Wabunge tukapimwe akili. Matokeo yake tukaletewa semina hapa ya matumizi sijui ya bangi, matumizi ya pombe, matumizi ya sigara, tukaonyeshwa udhaifu wake. Umbali kutoka hapa mpaka kwenda pale kwenye kituo cha wagonjwa wa akili kupima, siyo mbali. Hivi tunapata shida gani kwenda kupimwa akili sisi Wabunge? Kwa sababu inafika sehemu mtu anaongea lingine, anakupa mambo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nashangaa, hebu nendeni Majimboni kwenu kwanza halafu tuone kama utekelezaji wa ilani haufanyika katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuchangia kama ifuatavyo:-

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Angelina Malembaka kuna kanuni inavunjwa. Mheshimiwa Selasini.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama kwa mujibu wa Kkanuni ya 64 (1) (g). Mheshimiwa anasema Wabunge waende kupimwa akili. Sasa hii siyo akili nzuri. Kama yeye anajisikia akili yake ina matatizo, akapime. Sisi wengine hususan mimi, akili yangu ni nzuri kabisa ni timamu sihitaji kwenda kupima akili Milembe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ama afute kauli yake au usaidie afute kauli yake kwa sababu Bunge zima litaonekana kwamba sisi ni vichaa. Au athibitishe kwamba kuna Wabunge humu ambao wana akili ambazo siyo nzuri. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Selasini amesimama kuoneshwa kwamba kanuni ya 64 (1) (g) imefunjwa na Mheshimiwa Malembeka kwa kusema kwamba Waheshimiwa Wabunge akili.

Waheshimiwa Wabunge, ningetamani kama ambavyo huwa nasisitiza siku zote; moja, kuzingatia kanuni zetu; lakini la pili, ni uvumilivu. Haya mambo ya kupimwa akili, kuna wakati kuna Mbunge alishapata kusema Watanzania wote inabidi wakapimwe akili. Wakati huo haikuonekana kama ni jambo la ajabu Watanzania kuambiwa wakapime akili.

Wakati huo huo sisi Wabunge hapa ni Wawakilishi wa hao wananchi ambao tunawatuma ili wakapime akili. Sasa nakuwa sielewi ni wakati gani kipimo tayari kinakuwa kimeshajulikana kabla hatujaenda.

Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, tuwe tunafuatilia sisi wenyewe michango yetu na maneno tunayoyatumia. Maneno yale ambayo siyo lugha ya Kibunge, hayo yatakuwa yanaondolewa kila wakati. Yale ambayo matumizi yake huwa tunayatumia sisi wenyewe, basi tuwe wavumilivu hata vile ambavyo huwa yanatoka sehemu nyingine.

Mheshimiwa Malembeka, endelea na mchango wako. (Makofi)

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi, tunaendelea kusisitizana kupima afya zetu ikiwemo Malaria, UKIMWI, TB, vyote tukapime. Nasi Wabunge ni binadamu kama wengine, lazima tukacheki afya zetu kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumwambia Mheshimiwa Waziri wa Fedha kama nilivyosema mwanzo, wao mara zote wanachangia, wanakataa, wakishamaliza, wanakuja huku kuomba. Sasa hilo nanyi mliweke sawa, kwamba isifike sehemu sisi ambao tunakuja tunatetea hoja zetu, tunatete kauli zetu na yule ambaye kila siku anapinga, tena anapiga kwa uwazi, halafu tunaonekana wote tupo sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo Majimbo ambayo watu kila siku wanasimama hapa wanapiga kelele, lakini Majimbo yao hayajafanyiwa kazi.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Kuna wengine kila kitu wanakataa, lakini wanafanyiwa kazi. Mimi lengo langu kubwa ni kwamba kwa kuwa Ilani ya Chama cha Mapinduzi inatekelezwa nchi nzima, sasa…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Malembeka, kuna taarifa.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Sasa wasiwe kila kitu wanakataa. Vile ambavyo wamefanyiwa, wawe wanakubali kuwa…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Malembeka, kuna taarifa. Mheshimiwa Khatib.

TAARIFA

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nampa taarifa mwongeaji kwamba Wabunge wanapowafuata Mawaziri kuomba ni haki yao kwa sababu ni Serikali yao na kodi zinajumlisha Majimbo yao. Hivi ni nani bora...

NAIBU SPIKA: Taarifa ni moja Mheshimiwa Khatib. MHE. CECIL D. MWAMBE: (Aliongea nje ya microphone) NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Cecil, taarifa ni moja Mheshimiwa Khatib. Mheshimiwa Malembeka, endelea na mchango wako.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kesho ni siku ya kupiga kura na Watanzania wapo wanatuona. Hizo taarifa, taarifa zao wanazotaka kunivuruga ili nisimalize ninayosema, nitayasema mpaka dakika ya mwisho.

MHE. CECIL D. MWAMBE: (Aliongea nje ya microphone)

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilindie muda wangu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Malembeka naomba unyamaze kidogo.

Mheshimiwa Cecil Mwambe, Michango ya harusi sasa hivi inahusikaje? Hebu kuwa mtu mzima kidogo, tafadhali. Hebu kuwa mtu mzima kidogo for once tafadhali. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Angelina Malembeka endelea kuchangia na harusi ni wewe unapanga namna ulivyoona; na watu tuliokuchangia tumenyamaza, wanaopiga kelele hata hawakukuchangia.

Mheshimiwa Mbunge, endelea la mchango wako.

MBUNGE FULANI: Rudisha hela wewe mamaa!

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza, siwezi kuchanganyikiwa na kelele ya mtu yeyote kwa sababu havinihusu. Mimi ninaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono moja kwa moja mapendekezo ya Hotuba ya Waziri wa Fedha kwa sababu za kwanza zifuatazo:-

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza katika hotuba yao ya mapendelezo wameelezea kwamba wana nia nzuri ya kupanua wigo wa kodi na usajili wa walipa kodi. Pili, wameelezea nia yao ya dhati kuwekeza kwenye maeneo ambayo Serikali inaweza kupata mapato zaidi ikiwemo katika Sekta ya Uvuvi, ndani ya bahari kuu na ujenzi wa bahari za uvuvi lakini pia katika ununuzi wa meli za uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika mapendekezo hayo nimeona wamelezea ni jinsi gani ambavyo wanaweza wakaongeza ufanisi katika usimamizi na ukusanyaji wa kodi za ndani. Pamoja na hayo, wameonyesha kwamba wana nia ya dhati kabisa ya kuimarisha uwezo wa ufautiliaji na udhibiti wa uhamishaji wa faida na unaofanywa na makapuni ya nje. Pamoja na hilo, wameelezea nia yao ya dhati kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji na katika taasisi za Serikali ambazo zinatakiwa zitoe makato yao katika Mfuko Mkuu kwa muda muafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wameahidi na wameelezea kwamba wako tayari sasa hivi kuimarisha usimamizi wa misamaha ya kodi ambayo mapato yake yataenda katika miradi ambayo imekusudiwa. Mheshimiwa Waziri, mimi nataka niseme kidogo kwamba katika suala la kilimo yamezungumziwa mazao mengi ya mkakati. Naomba niwakumbushe, katika mazao ya mkakati, lipo zao la minazi ambalo wengi hawajalizungumzia. Zao lile ni zao ambalo lipo katika mikoa ya Pwani na limekuwa na faida nyingi sana ikiwemo masuala ya mapambo, mafuta yenyewe, urembo, dawa na kila kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wengi ambao wanavuna minazi sasa ni ile ambayo ilipandwa na mababu zao. Haijaoneshwa msimamo wakati sasa hivi kuonyesha na kuhamisha zao la minazi lipandwe nalo liingie katika biashara kama ilivyo mawese na mazao mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna suala la Wakandarasi. Wengi wana madeni na tulikuwa tunasisitiza Wakandarasi wa ndani wapewe fursa ya kuwekeza ndani, lakini madeni yale yamekuwa yanawakatisha tamaa. Utakuta wanadai miaka miwili mpaka mitatu. Naomba katika bajeti hii wawaangalie Wakandarasi waweze kulipwa fedha zao ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala zima la taulo za kike. Mimi naunga mkono kwamba kwa kuwa huku zinaingizwa kodi, halafu upande wa pili wawekezaji wa ndani wanapunguziwa kodi ili waweze kutengeneza taulo za kike, ni vizuri kwa sababu pamoja na kupunguza hizo gharama kwa wanafunzi na akina mama, lakini suala kubwa hapo kuangalia lisiwe kwenye suala la taulo tu tuangalie uwezekano wa kupata maji katika maeneo yao. Kwa sababu hata kama watapewa mataulo, hata kama kodi itapunguzwa, lakini ikiwa maji hamna katika maeneo yale, bado tutakuwa tuna hangaika. Kwa hiyo, suala la maji naomba liwekewe umuhimu sana katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la reli ya kisasa, wapo wanaolalamika kwamba ujenzi wa reli ya kisasa kwamba tunasaidia nchi nyingine badala ya kunufaika sisi Watanzania. Ninaamini kabisa, ujenzi wa reli ya kisasa utatoa ajira kwa Watanzania, lakini pia itatusaidia katika usafiri na katika kuinua uchumi wa nchi yetu. Hili jambo zuri na kubwa lazima lipongezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie suala la Madiwani. Tunao Madiwani ambao tunafanya nao kazi muda mrefu. Posho zao bado zimeendelea kuwa chini. Naomba katika bajeti hii tungalie Madiwani ili nao waweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja tunakutana kesho. (Makofi)
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba wenzangu wa upande wa pili wawe watulivu na hizo microphone wasiwe wanawasha kwa sababu sisi huwa hatuwashi. (Makofi)
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nachukua nafasi hii kumpongeza Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na timu yake yote. Pia nichukue nafasi hii kipekee kumpongeza Amiri Jeshi Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya. Kiaina nimpongeze aliyetengeneza kitabu hiki kwa kumwonesha komandoo akiwa kwenye mavazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mchango wangu kwenye Wizara hii kwanza naunga mkono kwa asilimia mia moja. Nichangie kwenye nyumba za askari. Nimeona juhudi za Wizara katika kujenga nyumba za askari. Naomba Serikali yangu tulivu iendelee kuwajengea nyumba askari hawa ili waweze kuishi vizuri na kufanya kazi zao kwa umakini zaidi. Nimeona maeneo mbalimbali ambapo nyumba zimejengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niombe Serikali yangu tulivu iendelee kuboresha maslahi ya askari wetu ikiwepo mishahara na vyombo ya usafiri. Niombe pia Wizara hii kwa nguvu za dhati ihakikishe mafunzo kwa askari wapya yanafanyika yakiwa yamelenga kada tofauti. Nimesikitishwa hapa na mwasilishaji wa Kambi ya Upinzani akishangaa Askari mstaafu kuwa mganga wa kienyeji. Mimi naamini kabisa kule kwenye uaskari siyo kwamba wana fani moja tu ya kushika bunduki na kucheza gwaride. Najua kabisa kule tunao Askari ambao ni wajasiriamali, wana ujuzi wa teknolojia mpya, wanahabari, wanamichezo, madaktari, madereva, marubani, walimu, mafundi umeme na waokoaji. Kwa hiyo, huyo Askari aliyeenda kuwa mganga wa kienyeji ndiyo fani yake usimlaumu.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia zaidi katika ajira. Naomba jeshi hili hasa Jeshi la Wananchi liangalie uwiano wa mikoa yote. Kuna baadhi ya maeneo imeonekana kama vile kuna kabila moja tu ndiyo jeshi hilo kazi yake mpaka inafika kipindi mitaani huko ukiwauliza JWTZ ni nini, wanakwambia ni Jeshi la Wakurya Toka Zamani.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba ajira zile ziangalie mikoa mbalimbali angalau ukikuta Wachaga kumi basi na Wamasai, Waluguru na Wapare wapo isiwe kabila moja ndio linafanya kazi ya jeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe pia Wizara hii iangalie ubunifu wa vijana wetu. Tunao vijana wengi ambao katika utundu wao wameweza kubuni redio, TV, simu mpaka helikopta. Ni vizuri jeshi hili likawachukua vijana wale na kuwapa mafunzo halafu baadaye wapate ajira. Nategemea kwa kufanya hivyo tutaendelea kuwa na vijana ambao watakuwa askari bora zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie pia katika kambi za jeshi. Najua wakati zinaanza zilikuwa nje ya mji lakini baadaye mji jinsi ulivyokua imeonekana kama vile vimeingiliana. Katika kuepuka madhara zaidi ya mabomu kama yale ya Gongo la Mboto na Mbagala au kuepuka migogoro ya ardhi kati Wanajeshi na raia lakini pia kuepuka migororo ambayo mingine inaingilia mipaka ya kimapenzi kati ya Askari na raia, ni vizuri basi tuangalie uwezekano wa kubadilisha makazi hayo. Mapori bado tunayo mengi, wahame kidogo waende kule ili wananchi waweze kukaa katika maeneo hayo kwa utulivu. Yapo maeneo ambayo hayawezekani kuhamishwa kutokana na hali halisi ilivyo basi wale ambao wanazunguka eneo lile wahamishwe kwa utaratibu unaofaa ili waweze kupisha jeshi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia hii itasaidia katika kujenga heshima ya jeshi. Imefika sehemu heshima ya jeshi inaanza kupungua kwa sababu wanajichanganya sana na raia. Katika kujichanganya na raia unakuta kuna mambo mengine ambayo Wanajeshi wanafanya unashangaa. Hata katika foleni za magari unakuta kwenye mchepuko na yeye anaingia, unatazama unaona ni Askari na ana kofia. Napenda zaidi Askari waoneshe wao wako makini na ni watii wa sheria, siyo wote wanaofanya hivyo ni baadhi. Wapo ambao pia wanakuwa wasumbufu katika maeneo ya watu yaani hata jirani yake anaogopa kukaa jirani na mjeshi. Naomba wale wachache wenye tabia kama hizo wabadilike. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nielezee kuhusu baadhi ya shule ambazo zinasimamiwa na jeshi zikiwepo shule binafsi nikitolea mfano Mgulani na Lugalo.
Kuna shule ambazo zimeendeshwa vizuri wanafunzi wa pale wanakuwa na maadili mazuri. Ni vizuri shule kama zile ziendelezwe na kupewa ushirikiano ili tuendelee kupata wanafunzi wenye nidhamu na wenye uchungu na nchi yao ambao hata kesho wakija huku Bungeni wataongea kwa kuitetea nchi yao siyo kuzomeazomea.
Mheshimiwa Naibu Spika, zamani tulikuwa na vyuo vya ualimu ambavyo vilikuwa vinasimamiwa na jeshi nikitolea mfano ya Monduli, Morogoro TC na Tabora Boys. Vyuo vile vilikuwa vinatoa walimu wenye nidhamu nzuri na wenye uchungu na nchi yao. Kama kuna uwezekano utaratibu ule urudishwe ili tuendelee kupata Wanajeshi ambao wanakuwa na fani tofauti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, siwezi kunyamaza kimya bila kusemea suala la uchaguzi wa Zanzibar. Tunakubali wote kwamba Amiri Jeshi Mkuu alisema, tena matangazo yalitoka kwenye televisheni, redio na magazeti kwamba yeye kama Amiri Jeshi Mkuu ana wajibu wa kulinda usalama Tanzania hii katika mkoa wowote siyo Dar es Salaam, Pemba au Mwanza na alimalizia kwa kusema atakayefanya fyokofyoko nitamshughulikia. Ukiona mtu analalamika kama alifanya fyokofyoko anashughulikiwa. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuonesha, kama angesema halafu wakanyamaza wangedharau wakasema amesema mbona hajafanya lolote, amesema na hawajathubutu kufanya fyokofyoko ndiyo maana wamenyamaza na kama watafanya fyokofyoko, Amiri Jeshi Mkuu aendelee kufanya kazi yake, ndiyo tutaendelea kuheshimiana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee zaidi katika suala zima la mafunzo ya kijeshi kwa vyama vya kisiasa. Kumekuwa na utaratibu wa baadhi ya vyama vya kisiasa kutengeneza makundi ya kijeshi kwa kujifanya kwamba wanalinda wakati wa kampeni au kulinda kura zao. Naomba jeshi lifanye kazi ya ziada, Mheshimiwa Waziri alisimamie, yapo makundi yanayojiita mazombe, wenyewe wanayajua huko ndiyo maana kila saa wanayataja, kuna makundi yanajiita blue guard yapo huko, yanafanya vituko kusingizia vyama vya siasa. Naomba Mheshimiwa Waziri yale…
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Green guard umetaja wewe sijataja mimi. Kwa hiyo, ninachoomba yale makundi yote yanayoendesha mafunzo ya kijeshi kwa kusingizia vyama wayadhibiti kwa sababu hayo ndiyo yanayotuletea fujo katika nchi yetu na kusababisha makundi ya wahalifu katika mitaa yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia 100 na wale waliobana sasa wameachia. Ahsante.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Malembeka wakati ukichangia, kuna tuhuma hapa umezitoa kuhusu ukabila jeshini. Kwa mujibu wa Kanuni ya 72(1) na Kanuni ya 64(1)(a), naomba ufute hayo maneno halafu tuendelee. (Makofi)
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilitolea mfano na nafuta kauli hizo.
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, na mimi naungana na wenzangu kumpongeza Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya. Nampongeza kwa dhati kwa sababu najua hii Wizara aliyoipata ambayo anaifanyia kazi mara nyingi amekuwa anaifanyia kwa vitendo. Nimemshuhudia mwenyewe Mheshimiwa Nape akipiga gitaa, nimemshuhudia mwenyewe Mheshimiwa Nape akiimba, nimemshuhudia mwenyewe Mheshimiwa Nape akicheza kiduku, nimemshuhudia Mheshimiwa Nape akicheza sindimba, nimemshuhudia Mheshimiwa Nape akicheza mayonjo, ina maana yuko kwenye fani. Nakupongeza sana Mheshimiwa Nape pamoja na Naibu Waziri wako. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utaenda kwa vifungu, kwanza nianze kidogo kwa mkwara tuliopigwa kwamba tukienda kucheza kwa King Kiki tutakuwa tumekula rushwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Afya wakati anawasilisha Bajeti yake alikuja na wanakijiji hapa akatuambia kijiji kile kina miaka mitano hakuna mama aliyefariki kutokana na uzazi, tukapiga makofi. Alipokuja Waziri wa Muungano na Mazingira alikuja na Waasisi wa Muungano akatuonesha tukapiga makofi, lakini pia, akatuonesha mwanafunzi Getrude Clement ambaye alituwakilisha Marekani kwenye masuala ya mazingira, tukapiga makofi. (Makofi)
Lakini pia alipokuja Waziri wa Biashara, Viwanda na Uwekezaji alituambia pale nje kuna wafanyabiashara wa magari wanaotaka kwenda kununua yako pale, tukapiga makofi. Pia Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa wakati anawasilisha mada yake hapo tuliwaona maafande wamejaa huku tele wa kila Idara tukapiga makofi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuko Wizara ya Habari, Utamaduni, Michezo na Sanaa, Waziri anaonesha wadau wake, tunaambiwa tukienda kucheza kwa King Kiki tunakula rushwa, hiyo haki kweli?
Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi King Kiki nimemjua nikisoma shule ya msingi, nikasoma sekondari, nikaolewa, nikacheza muziki kwa raha yangu, nimeingia Bungeni King Kiki yupo na akipiga ninaingia. Kwa sababu hiyo imeonesha jinsi gani wanamuziki wakongwe waliokaa hapa nchini na kufanya kazi zao bila kutetereka, sasa kama mtu amefanya shughuli ya muziki kwa kipindi kirefu, leo anakuja hapa kuonesha ujuzi wake na kuwafurahisha Wabunge, mnasema ni rushwa. Hivi mambo mangapi yanayofanyika humu ndani, mbona hamyasemi? Mmeona tu ya King Kiki kuja hapa kuwaburudisha Wabunge ndiyo imekuwa nongwa? Tubadilike! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaendelea kuzungumzia sekta ya habari. Kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza wamiliki wote wa vyombo vya habari hapa nchini bila kuwasahau wenzetu wa Gazeti la Uhuru na Mzalendo, pamoja na redio Uhuru. Pamoja na pongezi hizo kwa wanahabari na wamiliki wa vyombo vya habari nizungumzie maslahi ya wanahabari.
Mheshimiwa Mwenyekiit, wanahabari wengi mapato yao yako chini, wanahabari wanaweza wakapewa sehemu wakafuatilie kazi bila usafiri. Lakini wanahabari hawa pia bado tuna matatizo nao kwamba wana utaalamu wa kuandika pia habari potofu. Unaweza ukakuta taarifa ile ile kwenye gazeti hili unaambiwa sita wamekufa, hili saba wamekufa, lingine 10 wamekufa, na lingine watatu wamekufa, ajali ni ile ile moja, hilo pia ni tatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna tatizo la kutoa habari kwa upendeleo. tatizo hili tumeliona hasa kipindi cha uchaguzi na kipindi cha kampeni. Ni vizuri basi, zile taasisi za habari zijielekeze moja kwa moja kwamba tuko hivi, kama walivyofanya redio Uhuru na magazeti ya Uhuru kwamba, ukienda kule unajua wewe ni Chama cha Mapinduzi, vingine vimekaa kimya huku vinatoa habari kwa upendeleo. Tumeviona, tunavijua na tutavifanyia kazi maana Serikali ni yetu, Mheshimiwa Nape ni wetu na tutapambana. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siamini kabisa kama Mbunge utakaa ndani ya Bunge kwa miaka mitano, toka asubuhi mpaka jioni wanakuona kwenye tv kwenye Jimbo lako utapata maji, utapata zahanati, utapata shule, utapata barabara, utapata umeme hiyo siamini! Ninachoamini ni kwamba utakapokuja kwenye Bunge na kutoa hoja zako na kurudi kwenye Jimbo lako kwenda kutekeleza yale ya wananchi waliyokutuma ndipo utakapopata maendeleo na ndipo watakapokuchagua. Hawakuchagui kwa kuangaliwa kwenye tv. Ingekuwa kuangaliwa kwenye tv tunachaguliwa tusingeenda Majimboni kuomba kura. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kitu gani kinachong‟ang‟ania sana tu kwenda kwenye tv. Mmemzomea Rais hapa na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi tumenyamaza, mkatuona wajinga. Mkaendelea akaja Waziri Mkuu hapa mkakataa kusikiliza hotuba yake wala kuichambua, tukanyamaza kimya mkasusa mkatoka hatujawasemesha, lakini pia uchaguzi wa Zanzibar mmenuna, sisi tumepiga kura tumemalizika.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema ni kwamba, siku zote ninyi mkinuna wenzenu wanakula. Kununa mnanuna wenyewe halafu mnalalamika! Hakuna kitu chochote ambacho hakina mwanzo. Tuliingia kwenye Bunge vizuri, tulikuwa tunaonekana kwenye televisheni na kila mtu alikuwa anaona raha kuonekana kwenye televisheni, lakini haya mmeyataka ninyi wenzetu. Televisheni mmefanya ndiyo kituo cha kutukania viongozi wakubwa Serikalini, kutukania Marais, kukashifia Serikali iliyoko madarakani, hatuwezi kukubali. Kuna watu hawapendi ugomvi, kuna watu wameamua kujiweka sawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wameamua kujiweka sawa kwa maana kwamba, kitu kingine kama mtu hataki…
MWENYEKITI: Waheshimiwa naomba utulivu jamani tumsikilize Mbunge. Naomba nidhamu ndani ya Bunge, upande huu nimewasikia.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Kama mtu hataki siyo lazima apambane na wewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, usiwe na wasiwasi mimi nilishasema daktari aje apime watu akili. Kwa hiyo, usiwe na wasiwasi waache wazomee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani mtu toka asubuhi anatoka nyumbani anamuaga mke wake anakuja hapa kwa kazi ya kuzomea. Halafu analalamikia tv! Tv ya nini?
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi mimi nitakubali kweli mzazi wangu anatukanwa humu halafu nakubali. Hicho kitu hakiwezi kukubalika. Binafsi kama Mheshimiwa Malembeka siwezi kukubali kiongozi wangu anatukanwa humu televisheni na wote wanamuangalia, siwezi kukubali. Kwa sababu hata mzazi wako kama anatukanwa, ukihadithiwa tu unataka kupigana sembuse kuangalia. Hicho hatuwezi kukubali.
Taarifa....
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hiyo taarifa kwa sababu zifuatazo; Kwanza nina uhakika humu ndani kuna watu wameoana bila taratibu, wake zao nyumbani hawajui lakini hapa wanajifanya mke na mume, hilo la kwanza. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo ninaikataa kwa sababu mimi ninajua ndoa ya mkristo ni moja, siyo mbili wala tatu, lakini kuna watu humu wana wake, ambao wake zao hawajui, mbona hawaoneshi kwenye televisheni?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea, wasinipotezee muda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nirudi kuhusu suala la michezo. Kwanza nizungumzie suala la vifaa vya michezo, ninaomba bei zipungunzwe kwa sababu sasa hivi vijana wengi wamejikita kwenye michezo lakini vifaa bei iko juu. Ndiyo maana utakuta wakati mwingine wanacheza mpira bila viatu, kwa hiyo ni vizuri bei ya vifaa vya michezo zipunguzwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda nizungumzie Kijiji cha Michezo kilichopo Mvuti katika Kata ya Msongola, eneo lile limetengwa heka 10 kwa ajili viwanja vya michezo…
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Naungana na wenzangu kumpongeza Waziri wa Ardhi pamoja na Makamu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niungane na wenzangu kuzungumzia nyumba za bei nafuu ambazo siyo nafuu. Nilimsikia Mheshimiwa Waziri mwenyewe wakati anazungumza katika vipindi mbalimbali akizungumzia bei ya nyumba zinazoitwa nyumba nafuu, lakini siyo bei nafuu. Mimi naona kwa kuwa, yeye ameligundua hilo naomba alisimamie! Haiwezekani nyumba ya vyumba viwili ikauzwa milioni 70 halafu unasema ni nyumba ya bei nafuu! Hilo naomba alisimamie ili wananchi wetu wenye kipato kidogo waweze kufaidika na nyumba hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia, nizungumzie mradi wa viwanja eneo la Mvuti katika Manispaa ya Ilala. Tulihamasishwa, kwanza napenda ku-declare interest kwamba, nilishakuwa Diwani wa Kata ya Msongola, lakini pia, nimekuwa Diwani wa Kata ya Chanika kwa miaka 10 mfululizo ambako katika Kata hizo pia, imeweza kutoka Kata ya Majohe, Kata ya Buyuni na Kata ya Zingiziwa, kwa hiyo, nina uzoefu karibu katika Kata tano katika Jimbo la Ukonga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Mvuti tulihamasisha wananchi na wananchi walikubali kuingia katika mradi wa upimaji viwanja katika Mitaa ya Kidole, Sangara, Mkera na Luhanga, lakini tangu mradi ule wananchi walivyokubali hakieleweki nini kinachoendelea kwa sababu, wamekatazwa kulima na hawajengi, lakini mradi hauendelei!
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa wengi wameanza kukata mazao yao ikiwepo michungwa na miembe wakichoma mkaa wakitegemea kwamba, nyumba wakati wowote zinakuja, ili nao waishi kimjinimjini, lakini hali inakwenda taratibu. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja niweze kujua mradi wa viwanja katika Kata ya Msongola katika maeneo hayo niliyoyataja umefikia wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, napenda kujua taarifa kuhusiana na nyumba za Buyuni katika mradi wa viwanja elfu 20 vya Buyuni. Katika eneo hilo imehusisha mitaa ya Kigezi, Mbondole, Zavala na Vikongolo, kuna nyumba zaidi ya 2000 hazijulikani mwenyewe ni nani! Wengine wanasema Shibat wengine wanasema za Mchina! Katika nyumba hizo wanaoishi pale ni karibu watu 20 tu maeneo yaliyobaki yamerudi tena kuwa pori! Sasa zile nyumba sasa hivi zimeshakuwa zina mgogoro kwa maana kwamba, zinawapa matatizo wananchi! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yale watu wanabakwa, maeneo yale wezi wanakwenda kujificha, lakini maeneo yale tena yameshakuwa, mtu huwezi kupita jioni kwa sababu, nyumba ziko nyingi wanaoishi ni wachache, mapori yamerudi tena na nyumba zile hazijulikani mwenyewe nani na kwa nini watu hawakai, lakini kwa uchunguzi wa haraka tumeambiwa kwamba, zile nyumba pamoja na kwamba, zimekamilika bei ni kubwa sana ndiyo maana wananchi hawakai! Sasa majengo yamejengwa yako tupu yanaendelea kuharibika! Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atueleze nyumba zile ni za nani na kwa nini hawahamii mpaka sasa hivi wakati zimekamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia suala la Kazimzumbwi. Kazimzumbwi inagusana na Mitaa ya Kigogo, Kimwani, Nyeburu, Nzasa na Ngobeje. Hapa naomba niongee kwa kina. Suala la mgogoro wa ardhi wa Msitu wa Kazimzumbwi na wananchi wa Kata ya Chanika haujaanza jana wala juzi, ni wa muda mrefu, lakini niseme wanasiasa tunazidisha sana mgogoro ule kuufanya usimalizike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshiriki vikao mbalimbali vya kutatua mgogoro ule, lakini utakuta wakati wa uchaguzi ukifika wagombea wa vyama mbalimbali wanaenda kuwashawishi wananchi msikubali, msifanye hivi. Kwa hiyo, kunakuwa na vurugu, zile Kamati hazifiki mwisho, uchaguzi ukiisha yanakwisha, uchaguzi ukikaribia vurugu zinaanza tena. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa sasa hivi uchaguzi umekwisha, hatuna uchaguzi wa Serikali za Mitaa, hatuna uchaguzi wa Mbunge, aende kule akafanye kazi ili wale wananchi wawe na jibu la uhakika badala ya kuwa na majibu ya kisiasasiasa. Huyu anakuja asubuhi anasema nendeni, huyu anakuja anasema toeni. Naomba kwa kipindi hiki akafanye kazi tuje na jibu kuhusiana na Msitu wa Kazimzumbwi na wananchi wa Kata ya Chanika na mitaa husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie tena suala la mashamba pori. Mara nyingi limekuwa linazungumziwa kwamba mashamba pori yachukuliwe lakini bado haujatolewa mwongozo wananchi wanayachukua kwa utaratibu gani? Kuna wananchi wakishasikia huku Bungeni mmesema mashamba pori marufuku, wanavamia mashamba, wanakamatwa, wengine wanapigwa na wengine wanapelekwa mahakamani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba wanapotoa mwongozo kwamba yale mashamba makubwa yachukuliwe, watoe na ufafanuzi wanachukua kwa utaratibu gani ili wananchi wasipate matatizo. Wakati huohuo kuna mashamba makubwa ambapo wamiliki wana hati zao na wameyanunua kwa ajili ya kujenga shule, zahanati au hosteli kwa siku zijazo. Kwa hiyo, ni vizuri basi masuala haya yawe yanatolewa ufafanuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kumaliza kuongea kabla sijazungumzia viwanja vya CCM. Kuna watu hapa wakikaa wanazungumzia CCM ina viwanja, ni vyetu. Utaratibu wa Chama cha Mapinduzi huwezi kujenga tawi kama huna kiwanja ambacho ni halali. Kwa hiyo, kila tawi lazima lihakikishe uhalali wa kiwanja chake ndipo linaitwa tawi Ukiona tawi ina maana lina wanachama si chini ya 50. Unapoona Tawi la Mjumbe wa Shina ina maana si chini ya wanachama 10.
Sasa mtu anakuja anakaa mwenyewe anazunguka tu viwanja vyote vya CCM, viwanja vyote ni vya CCM, ni vya kwetu, ni vya halali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri, wale wote kupitia Chama cha Mapinduzi watakaoleta maombi ya kupata hati ya viwanja vyao alifanyie kazi ili Chama cha Mapinduzi viwanja vyake viweze kuwa na hati.
Maana kuna watu wana uchu yaani mtu anasimamisha bendera moja….
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na uendelea kunilindia muda wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ni kwamba mara zote anayeanza kusema anaonekana mwema wa mwisho anamalizia. Nasema viwanja vya Chama cha Mapinduzi visiwatie presha ni vyetu! Kama mnataka viwanja vingi njooni ndani ya Chama cha Mapinduzi mtapata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tena bahati nzuri au bahati mbaya ndani ya Chama cha Mapinduzi ukiona Mjumbe wa Shina kaweka bendera moja ina maana ana watu 10, ukiona tawi lina bendera moja lina watu zaidi ya 50, tofauti na vyama vingine yaani mtu mmoja anapata uongozi bendera 200 zinamwagwa.
Naomba muelewe kwamba Chama cha Mapinduzi viwanja vyake ni vya halali hatujaiba. Kama kuna mtu ana uhakika tumeiba aende mahakamani, tutapambana naye. Namwomba kwa mara nyingne Mheshimiwa Lukuvi, maombi yote ya Chama cha Mapinduzi kwa ajili ya hati za viwanja vya Chama cha Mapinduzi ayasimamie kama kawaida kwa sababu wale maombi yao ni halali siyo kwa wizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja kwa sababu wale Mawaziri ambao wako kwenye Wizara hii wanajiamini wanaweza kufanya kazi na wana uwezo wa kutoa maamuzi, siyo watu wa kuyumbayumba. Akisema bomoa, bomoa, jenga, jenga na huo ndiyo msimamo wa kiongozi, lazima uwe unaeleweka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa Fedha na Naibu wake pamoja na timu yake yote kwa kazi nzuri wanazozifanya na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kukupongeza wewe kwani katika filamu inayoendelea ndani ya ukumbi huu, wewe ndio nyota wa mchezo. Nikuhakikishie siku zote sterling huwa hauwawi, akiuawa ujue picha imekwisha. Kwa hiyo, naendelea kukupa moyo, endelea kufanya kazi mpaka tarehe 1 Julai na wewe ndiyo kipepeo wa jengo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza bajeti hii kwa sababu imeweka vipaumbele katika afya, elimu, maji na miundombinu na wenzangu wamechangia vizuri na mimi naomba niongeze nyama katika yale waliochangia wenzangu.
Kwanza niishauri Serikali yangu sikivu kwamba bajeti hii ilivyopangwa naomba fedha hizo zipelekwe kwa muda muafaka. Kumekuwa na tabia ya kupanga vitu tunashangilia halafu hela haziendi kwenye maeneo husika na zikienda zinaenda zikiwa zimechelewa na wakati mwingine zinafika kidogo. Sasa ili kutekeleza yale ambayo tumeyapanga hapa, ni vizuri fedha hizo zikapelekwa kwa wakati muafaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tuikumbuke ile miradi kiporo. Iko miradi ambayo sasa hivi imekuwa magofu na kila anayesimama anataja kwenye Jimbo lake, kwenye Wilaya yake. Naona ni vizuri sasa viporo hivyo tuvikamilishe ili hadithi ile ya kuhadithia tena, iwe imekamilika na isiadithiwe tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, ipo miradi ambayo imeanzishwa kwa nguvu au michango ya wananchi. Tumehamasisha wananchi wamajitolea na wamejenga hadi walipofikia lakini Serikali bado haijapeleka hizo fedha kwa ajili ya kukamilisha miradi hiyo. Naomba Serikali ipeleke hizo fedha ili kuwatia nguvu wananchi ambao wamejitolea kwa namna mbalimbali kuikubali miradi ile na kuichangia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la ukusanyaji wa mapato kupitia kodi za majengo. Katika hili, naomba tathmini ifanyike upya kwa baadhi ya maeneo. Mfano kuna nyumba yangu moja iko Chanika ndani ya plot moja lakini nimeletewa karatasi tatu. Nyumba yenyewe ina karatasi yake, banda la kuweka gari lina karatasi yake na choo cha nje kina karatasi yake. Sasa najiuliza hapa nikalipe nini, kuna nyumba isiyokuwa na choo nje au nikalipe choo tu nyumba niache, au nilipe banda la gari nyumba niache au nikalipe banda la kuku nyumba niache? Siyo hiyo peke yake, nimeona katika nyumba yangu ya Mvuti jiko la nje nalo nimepewa karatasi yake, sasa najiuliza hiyo tathmini ilifanywaje, kwa kuangalia sura ya mtu au kwa majina?
Naomba katika maeneo kama hayo tathmini ifanyike upya, wananchi wako tayari kulipa kodi ya majengo na sisi viongozi tuko tayari kulipa kodi ya majengo lakini iende kihalali. Yapo maeneo ambayo kuna nyumba ya vyumba viwili havijapigwa plasta lakini anaambiwa alipe shilingi 36,000 wakati mwingine ana vyumba vinne vina tiles, bati la South Africa anaambiwa alipe shilingi 21,000, hivi tathmini hiyo inapigwaje? Ni vizuri tujipange upya ili kutekeleza suala hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala hilo hilo la ukusanyaji wa kodi ya majengo na mimi naungana na wenzangu kuomba Halmashauri ziachiwe kukusanya. Hii ni kutokana na ukweli kwamba yapo mambo ambayo tumekubaliana kwamba mambo haya yatafanywa na Halmashauri, tutakapochukua kodi ya majengo, tutakuwa tunaziua zile Halmashauri na yale ambayo tumewapangia wafanye watashindwa kuyafanya. Kama tumekubaliana kuwapa mamlaka basi tuwape na madaraka ili waweze kufaya kazi vizuri. Halmashauri zimejipanga na zimeishafanya utafiti wa kutosha na wako tayari kwa ajili ya kukusanya fedha hizo za majengo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia kwenye suala la vivuko. Yapo majimbo mengi ambayo yamelalamikia vivuko na yakitaja viongozi mbalimbali wa zamani kwamba waliahidi kuvikamilisha lakini havijakamilika. Yapo maeneo ya Mafia, Bukoba, Ukerewe katika Ziwa Victoria, Ziwa Nyasa, Ziwa Tanganyika lakini pia bila kusahau Visiwa vya Unguja na Pemba. Wenzetu hawa suala la boat au meli ndiyo chombo kikubwa cha usafiri kwao. Kwa hiyo, yapo mambo ya kusubiri, lakini mengine inabidi tuyafanyie kazi mapema ili wenzetu twende nao pamoja. Kila nikifikiria mimi msiba wa MV Bukoba na MV Spice, bado najiuliza kwa nini mpaka leo hii meli nyingine hazijanunuliwa, naomba hilo tulifanyie kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala la michezo. Imefika sehemu hizi timu zinakuja kuonekana kama ni za mtu binafsi wakati zinawakilisha nchi. Inafika sehemu timu ya ngumi, netball, riadha, mpira wa miguu, kuogelea, unaambiwa imeshindwa kwenda kambini au imeshindwa kusafiri kwenda kuiwakilisha nchi kwa sababu hakuna pesa, sasa sijui tunajipangaje? Ndiyo maana wale wanaojitolea wachache kusafirisha timu wanajifanya wao maarufu sana na wanajifanya wao ndiyo wanazijua sana hizi timu kuliko Serikali, naomba Serikali zile safari za nje iwe inazigharamia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, naomba pia nichangie kuhusiana na ahadi za viongozi. Kuna ahadi za viongozi ambazo wamezitoa katika kampeni, zinavyojirudia mara tatu, mara nne, mara tano kwa awamu tofauti, ile tu siyo aibu kwa Serikali lakini pia ni aibu kwa chama chetu ambacho kimeongoza kwa kipindi chote. Naomba katika awamu hii zile ahadi zote zilizoahidiwa na viongozi waliopita zifanyiwe kazi ili tuendelee kuwapa imani wananchi na pia kuwahakikishia kuwa Chama cha Mapinduzi hakidanganyi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa ili nisipoteze muda, napenda kuzungumzia suala la kukata kodi ya kiinua mgongo kwa Wabunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, wapo waliotetea majimbo, mimi ni Mbunge wa Viti Maalum nawakilisha Mkoa mzima, misiba huko mkoani tunaijua, mipira ya huko mikoani tunaijua, michango ya huko mikoani tunaijua, tuna matatizo chungu mzima. Kama kukatwa kodi tulishakatwa kwenye mishahara na ipo michango mbalimbali ambayo Wabunge tunatakiwa tuitoe na huwa tunaitoa. Mpaka tunapofika dakika ya mwisho tunajipanga kwa ajili ya uchaguzi mwingine, naweza nisiwe mimi lakini akaja mtu mwingine, mnapokuja kumkwangua Mbunge moja kwa moja atasaidiaje yule mgombea wa chama chake ili aweze kuingia? Hakuna uchaguzi usiokuwa na gharama, chaguzi zote zina gharama, ndiyo maana hata Serikali huwa inajipanga.
Sasa mimi niombe, suala la kukata kiinua mgogo kodi ya Wabunge litafakariwe upya na tuangalie jinsi gani ya kulifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili niweze kutoa nafasi kwa wengine tena, naendelea kukupongeza kwamba wewe ndiyo nyota wa mchezo, ahsante kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniapa nafasi na niungane na wenzangu wote kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote wawili, Naibu Mawaziri wote wawili na Watendaji wao wote katika Wizara zao. Pamoja na pongezi zao hizo kipekee naomba niwapongeze madereva wao wote, wahudumu wao wote, na masekretari wao wote ambao wamefanya kazi hadi na wao wakaweza kuwakilisha hapa sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango wangu naomba nianze na Usalama wa Taifa. Mwaka jana wakati nachangia nilizungumzia suala la Usalama wa Taifa na hoja kuu ilikuwa suala la kutekwa nyara, nilisema hapa kutekwa nyara siyo mchezo, wengine wanajifungia ndani halafu wanapiga simu wametekwa nyara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikasema naomba sehemu hii iongezewe pesa ili waweze kupata mafunzo zaidi na kununua vifaa zaidi vya kisasa, nafikiri kwa kufanya hivyo tutaweza kupunguza suala la kupekuliwa pekuliwa asubuhi, kuvuliwa nguo, kuvuliwa viatu na hata kufikia kwenye sehemu ya kwamba tunakuwa na wasiwasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za karibuni tumejionea jinsi watu wanavyojiteka nyara wenyewe na kufanya hii Idara ionekane kwamba haifanyi kazi wakati Idara hii inafanya kazi vizuri. Niombe Idara hii iendelee kuongezewa pesa ili wapate mafunzo zaidi na vitendea kazi ambavyo hata sisi vitatusaidia kutovuavua mikanda pale mlangoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, napenda nichangie kuhusiana na maadili ya Viongozi wa Umma, Sekretarieti ya Viongozi wa Umma wanafanya kazi vizuri sana wamekuwa wepesi sana wa kutukumbusha kujaza fomu ni vizuri pia. Katika kutukumbusha kujaza fomu basi kama kuna kitu kinatakiwa basi wakiingize kabisa pale ili tunavyorudisha zile fomu twende nazo sambamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sekretarieti hii iongezeke zaidi badala ya kuangalia tu zile fomu twende kwenye neno kamili Maadili ya Viongozi, kama watavuka kufikia huko nafikiri hakuna Kiongozi atakayeitwa na Mheshimiwa Makonda hapa, hakuna Kiongozi atakayepelekwa Ustawi wa Jamii, hakuna Kiongozi tutakayemwona huko mitaani anatangazwa kwenye magazeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wajitanue zaidi wapewe pesa wajitanue zaidi watufuatilie kweli Viongozi maadili ni kweli au ni fomu tu hizo za kuhakiki mali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa. Idara hii imekuwa inafanya kazi vizuri, niipongeze Serikali kwa kuboresha majengo yao yote, wamefanya kazi vizuri sana, sasa hivi majengo yale matunzo yanaonekana, vifaa vinatunzwa kisasa na wafanyakazi wako kwenye amani. Hata hivyo, hawana pesa za kutosha kwa ajili ya kufanya tafiti mbalimbali na kuweza kupata kumbukumbu mpya na nyaraka mpya ambazo nyingine ziko mikononi mwa watu huko vijijini. Kuna watu wana historia ya nchi hi, kuna watu wana kumbukumbu nzuri lakini wanashindwa kuzileta. Ni vizuri basi wakaongezewa pesa ili wafanye utafiti wa kina na kwenda kwenye maeneo mbalimbali ili tuweze kupata kumbukumbu nyingine na kupata nyaraka nyingine ambazo bado ziko mikononi mwa watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia kuhusiana na suala la utawala bora. Kazi imefanyika vizuri niwapongeze sana, lakini kuna baadhi ya Halmashauri kazi haziendi. Vikao vya Halmashauri vya kikanuni haviendi vimekuwa vikikatizwa mara kwa mara na wengine wanaitwa tu kipindi cha kupitisha bajeti sasa hii imekuwa ni tatizo. Tatizo la posho liko palepale, Diwani anaidai Halmashauri, Diwani utaidaije Halmashauri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naona Halmashauri zijipange, tunategemea kwamba tuna Wakurugenzi wazuri ambao ni wabunifu, basi waendelee kubuni mbinu mbalimbali ya kujipatia pesa ili kuweza kuziendesha zile Halmashauri, pia kuondokana na migogoro ya madiwani. Posho ya Madiwani pia ni ndogo, tunazungumza mara nyingi jamani mishahara ya watumishi tuongeze lakini haijazungumziwa Madiwani. Madiwani ni muda mrefu wanafanya kazi na posho ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi hiki miezi mitatu yote Wabunge tuko Bungeni, lakini Madiwani bado wako na wananchi, shida za wananchi wanazo Madiwani, lakini bado posho iko vilevile, nimwombe Mheshimiwa Waziri waliangalie hili kuhusu posho ya Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine tena ambalo limezungumziwa juu ya kujipanga kwa ajili ya chaguzi za Serikali za Mitaa 2019. Nimefurahi kwamba mmeliona mapema na mmejipanga. Hata hivyo, wakati tunalipanga hili tuangalie kuna Kata nyingine, Mitaa mingine na Majimbo mengine ni makubwa kuliko tunavyofikiria. Kuna mitaa ambayo ina watu 10,000, nikitolea mfano katika Kata ya Msongola kuna mtaa wa Yangeyange una watu zadi ya 10,000, kuna mtaa wa Mbondole una zaidi ya watu 6000, sasa huo unakuwa mtaa au unakuwa kata. Ni vizuri basi wakati tunapanga uchaguzi huu wa mwaka 2019, basi waangalie jinsi gani ya kupunguza baadhi ya mitaa baadhi ya Kata na baadhi ya Majimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia kuhusiana na uchelewaji wa fedha za maendeleo katika Halmashauri, kwa kweli hiki ni kikwazo kikubwa sana ambacho hata Wabunge tunapoenda kwenye miradi mbalimbali kukagua huwa tunashikwa na butwaa kwamba tumepitisha pesa, wale wako tayari kufanya kazi lakini pesa haziendi. Basi ni vizuri tunavyoidhinisha kwamba pesa fulani ziende basi ziende kwa wakati na ikiwezekana ziende zikiwa zimekamilika ili miradi ile iweze kukamilika mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la TASAF na MKURABITA;, TASAF na MKURABITA imesaidia sana wananchi, sasa hivi wako katika mazingira mazuri sana, tumeangalia katika awamu ya tatu ya TASAF uwezeshaji wa wananchi kiuchumu wananchi sasa hivi wengi wameweza kupeleka watoto shule, wameweza kupeleka watoto kwenye zahanati na wameweza kubuni miradi mbalimbali ambayo inawaongezea kipato na hivyo kuwanyanyua kiuchumi. Ni vizuri basi hii sehemu ya TASAF ziongezewe pesa na ziende kwa wakati ili waweze kufanya kazi vizuri wananchi waweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika MKURABITA kazi imefanyika vizuri na akinamama wengi safari hii wameweza kunufaika na MKURABITA. MKURABITA vijana hawajanufaika, naomba utaratibu upangwe ili vijana nao waweze kunufaika katika mradi mzima wa MKURABITA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa nizungumzie kuhusu TARURA niipongeze kwanza TANROADS kwamba imefanya kazi nzuri katika barabara kuu, barabara ni nzuri zinapitika, lakini huku kwenye TARURA bado pesa ni ndogo za kufanyia kazi barabara zile ni nyingi na fedha ni ndogo, kama ingewezekana tufanye mageuzi mazuri TANROADS wapewe asilimii 30, TARURA wapewe asimia 70 ili zile kazi za TARURA ziweze kuonekana kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia kuhusiana na taulo za kike. Taulo za kike limekuwa gumzo, lakini wachache ambao wamekubali kuwa wawazi, wapo akinadada ambao ni wasichana wanashindwa kabisa kwenda shule wanapofikia katika siku zao kutokana na kukosa taulo za kike. Wengine wanaamua kujistiri hata kwa majani au matambala mabovu ilimradi tu aende shule, yule mwenye moyo mdogo akifikia hali ile anaamua kotokwenda shule kabisa na hivyo kufanya mtoto wa kike ashindwe kuhudhuria masomo na kupoteza mwelekeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kupitia Wizara yake azishauri Halmashauri, tunayo mikoa ambayo inalima pamba na kama inalima pamba na sasa hivi tuna Tanzania ya viwanda, kwa nini ile mikoa isitengeneze viwanda vidogovidogo vya kutengeneza hizo pamba angalau za kuwastiri akinadada halafu ziuzwe kwa bei nafuu au ikiwezekana zitolewe bure kwa wanafunzi ili waweze kushiriki vizuri masomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nitoe shukrani zangu na pongezi kwa Wenyeviti wangu wa Kamati wote wawili, wameonesha ushirikiano mzuri, kubwa zaidi kwa kuwa mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, niseme kwamba Mawaziri wetu wanashaurika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniapa nafasi na niungane na wenzangu wote kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote wawili, Naibu Mawaziri wote wawili na Watendaji wao wote katika Wizara zao. Pamoja na pongezi zao hizo kipekee naomba niwapongeze madereva wao wote, wahudumu wao wote, na masekretari wao wote ambao wamefanya kazi hadi na wao wakaweza kuwakilisha hapa sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango wangu naomba nianze na Usalama wa Taifa. Mwaka jana wakati nachangia nilizungumzia suala la Usalama wa Taifa na hoja kuu ilikuwa suala la kutekwa nyara, nilisema hapa kutekwa nyara siyo mchezo, wengine wanajifungia ndani halafu wanapiga simu wametekwa nyara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikasema naomba sehemu hii iongezewe pesa ili waweze kupata mafunzo zaidi na kununua vifaa zaidi vya kisasa, nafikiri kwa kufanya hivyo tutaweza kupunguza suala la kupekuliwa pekuliwa asubuhi, kuvuliwa nguo, kuvuliwa viatu na hata kufikia kwenye sehemu ya kwamba tunakuwa na wasiwasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za karibuni tumejionea jinsi watu wanavyojiteka nyara wenyewe na kufanya hii Idara ionekane kwamba haifanyi kazi wakati Idara hii inafanya kazi vizuri. Niombe Idara hii iendelee kuongezewa pesa ili wapate mafunzo zaidi na vitendea kazi ambavyo hata sisi vitatusaidia kutovuavua mikanda pale mlangoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, napenda nichangie kuhusiana na maadili ya Viongozi wa Umma, Sekretarieti ya Viongozi wa Umma wanafanya kazi vizuri sana wamekuwa wepesi sana wa kutukumbusha kujaza fomu ni vizuri pia. Katika kutukumbusha kujaza fomu basi kama kuna kitu kinatakiwa basi wakiingize kabisa pale ili tunavyorudisha zile fomu twende nazo sambamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sekretarieti hii iongezeke zaidi badala ya kuangalia tu zile fomu twende kwenye neno kamili Maadili ya Viongozi, kama watavuka kufikia huko nafikiri hakuna Kiongozi atakayeitwa na Mheshimiwa Makonda hapa, hakuna Kiongozi atakayepelekwa Ustawi wa Jamii, hakuna Kiongozi tutakayemwona huko mitaani anatangazwa kwenye magazeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wajitanue zaidi wapewe pesa wajitanue zaidi watufuatilie kweli Viongozi maadili ni kweli au ni fomu tu hizo za kuhakiki mali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa. Idara hii imekuwa inafanya kazi vizuri, niipongeze Serikali kwa kuboresha majengo yao yote, wamefanya kazi vizuri sana, sasa hivi majengo yale matunzo yanaonekana, vifaa vinatunzwa kisasa na wafanyakazi wako kwenye amani. Hata hivyo, hawana pesa za kutosha kwa ajili ya kufanya tafiti mbalimbali na kuweza kupata kumbukumbu mpya na nyaraka mpya ambazo nyingine ziko mikononi mwa watu huko vijijini. Kuna watu wana historia ya nchi hi, kuna watu wana kumbukumbu nzuri lakini wanashindwa kuzileta. Ni vizuri basi wakaongezewa pesa ili wafanye utafiti wa kina na kwenda kwenye maeneo mbalimbali ili tuweze kupata kumbukumbu nyingine na kupata nyaraka nyingine ambazo bado ziko mikononi mwa watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia kuhusiana na suala la utawala bora. Kazi imefanyika vizuri niwapongeze sana, lakini kuna baadhi ya Halmashauri kazi haziendi. Vikao vya Halmashauri vya kikanuni haviendi vimekuwa vikikatizwa mara kwa mara na wengine wanaitwa tu kipindi cha kupitisha bajeti sasa hii imekuwa ni tatizo. Tatizo la posho liko palepale, Diwani anaidai Halmashauri, Diwani utaidaije Halmashauri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naona Halmashauri zijipange, tunategemea kwamba tuna Wakurugenzi wazuri ambao ni wabunifu, basi waendelee kubuni mbinu mbalimbali ya kujipatia pesa ili kuweza kuziendesha zile Halmashauri, pia kuondokana na migogoro ya madiwani. Posho ya Madiwani pia ni ndogo, tunazungumza mara nyingi jamani mishahara ya watumishi tuongeze lakini haijazungumziwa Madiwani. Madiwani ni muda mrefu wanafanya kazi na posho ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi hiki miezi mitatu yote Wabunge tuko Bungeni, lakini Madiwani bado wako na wananchi, shida za wananchi wanazo Madiwani, lakini bado posho iko vilevile, nimwombe Mheshimiwa Waziri waliangalie hili kuhusu posho ya Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine tena ambalo limezungumziwa juu ya kujipanga kwa ajili ya chaguzi za Serikali za Mitaa 2019. Nimefurahi kwamba mmeliona mapema na mmejipanga. Hata hivyo, wakati tunalipanga hili tuangalie kuna Kata nyingine, Mitaa mingine na Majimbo mengine ni makubwa kuliko tunavyofikiria. Kuna mitaa ambayo ina watu 10,000, nikitolea mfano katika Kata ya Msongola kuna mtaa wa Yangeyange una watu zadi ya 10,000, kuna mtaa wa Mbondole una zaidi ya watu 6000, sasa huo unakuwa mtaa au unakuwa kata. Ni vizuri basi wakati tunapanga uchaguzi huu wa mwaka 2019, basi waangalie jinsi gani ya kupunguza baadhi ya mitaa baadhi ya Kata na baadhi ya Majimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia kuhusiana na uchelewaji wa fedha za maendeleo katika Halmashauri, kwa kweli hiki ni kikwazo kikubwa sana ambacho hata Wabunge tunapoenda kwenye miradi mbalimbali kukagua huwa tunashikwa na butwaa kwamba tumepitisha pesa, wale wako tayari kufanya kazi lakini pesa haziendi. Basi ni vizuri tunavyoidhinisha kwamba pesa fulani ziende basi ziende kwa wakati na ikiwezekana ziende zikiwa zimekamilika ili miradi ile iweze kukamilika mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la TASAF na MKURABITA;, TASAF na MKURABITA imesaidia sana wananchi, sasa hivi wako katika mazingira mazuri sana, tumeangalia katika awamu ya tatu ya TASAF uwezeshaji wa wananchi kiuchumu wananchi sasa hivi wengi wameweza kupeleka watoto shule, wameweza kupeleka watoto kwenye zahanati na wameweza kubuni miradi mbalimbali ambayo inawaongezea kipato na hivyo kuwanyanyua kiuchumi. Ni vizuri basi hii sehemu ya TASAF ziongezewe pesa na ziende kwa wakati ili waweze kufanya kazi vizuri wananchi waweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika MKURABITA kazi imefanyika vizuri na akinamama wengi safari hii wameweza kunufaika na MKURABITA. MKURABITA vijana hawajanufaika, naomba utaratibu upangwe ili vijana nao waweze kunufaika katika mradi mzima wa MKURABITA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa nizungumzie kuhusu TARURA niipongeze kwanza TANROADS kwamba imefanya kazi nzuri katika barabara kuu, barabara ni nzuri zinapitika, lakini huku kwenye TARURA bado pesa ni ndogo za kufanyia kazi barabara zile ni nyingi na fedha ni ndogo, kama ingewezekana tufanye mageuzi mazuri TANROADS wapewe asilimii 30, TARURA wapewe asimia 70 ili zile kazi za TARURA ziweze kuonekana kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia kuhusiana na taulo za kike. Taulo za kike limekuwa gumzo, lakini wachache ambao wamekubali kuwa wawazi, wapo akinadada ambao ni wasichana wanashindwa kabisa kwenda shule wanapofikia katika siku zao kutokana na kukosa taulo za kike. Wengine wanaamua kujistiri hata kwa majani au matambala mabovu ilimradi tu aende shule, yule mwenye moyo mdogo akifikia hali ile anaamua kotokwenda shule kabisa na hivyo kufanya mtoto wa kike ashindwe kuhudhuria masomo na kupoteza mwelekeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kupitia Wizara yake azishauri Halmashauri, tunayo mikoa ambayo inalima pamba na kama inalima pamba na sasa hivi tuna Tanzania ya viwanda, kwa nini ile mikoa isitengeneze viwanda vidogovidogo vya kutengeneza hizo pamba angalau za kuwastiri akinadada halafu ziuzwe kwa bei nafuu au ikiwezekana zitolewe bure kwa wanafunzi ili waweze kushiriki vizuri masomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nitoe shukrani zangu na pongezi kwa Wenyeviti wangu wa Kamati wote wawili, wameonesha ushirikiano mzuri, kubwa zaidi kwa kuwa mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, niseme kwamba Mawaziri wetu wanashaurika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Naungana na wenzangu wote kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake yote, kipekee naomba nimpongeze Mkuu wa Majeshi kwa kutambua umuhimu wa Wakuu wa Majeshi wastaafu ambao amewaalika. Hii inaonesha jinsi gani wapo tayari kushirikiana na kuendeleza amani iliyopo nchini mwetu na inatoa faraja sana kwa kuona ushirikiano uliopo inaonesha kwamba Tanzania bado tupo salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao vijana kadhaa wa JKT waliopo katika kambi mbalimbali nchini mwetu, vijana hao wamefanya kazi ya kujitolea kwa muda mrefu. Naiomba Serikali ajira zinapotokea basi wale wawe wa kwanza kuajiriwa kwa sababu wamefanya kazi ya kujitolea kwa muda mrefu. Hii itawasaidia kujenga uzalendo na hivyo kuendelea kuitetea nchi yao badala ya kuendelea kuwaweka pale muda mrefu na kuwakatisha tamaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuwapongeza SUMA JKT kwa kazi nzuri wanayoifanya. SUMA JKT wanafanya kazi nzuri na kwa bei nafuu sana. Nimeweza kuona majengo yao katika Zahanati ya Kiboga, Kata ya Msongola, Manispaa ya Ilala, lakini pia nimeweza kuona majengo waliyojenga katika Shule ya Sekondari Nyakato Mkoani Kagera na gharama yao ni ndogo na majengo ni mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali isiwe inawakopa SUMA JKT, wawe wanawalipa pesa zao zote na kwa wakati muafaka, hasa ukizingatia kwamba katika malipo yao wanaondoa faida na pia wanaondoa ile gharama ya vibarua, badala ya kuleta labour charge wao wanaleta labour force. Kwa hiyo, ni vizuri walipwe mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuishauri Serikali yangu sikivu kuhusiana na suala hilo hilo la SUMA. Vifaa vingi kwa kuwa SUMA JKT wanajitolea na wanafanya kazi nzuri basi hata maofisini kwetu tuwe tunachukua vifaa kutoka SUMA na majengo yetu yawe yanajengwa na SUMA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie katika suala la utumiaji wa silaha za moto vibaya, limekuwa ni tatizo kubwa nchini. Wakati huo huo niipongeze Serikali kwa kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali wameweza kulimaliza tatizo hili katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono suala zima la kununua silaha za kisasa zaidi, kutoa mafunzo zaidi na kuwawezesha wapiganaji wetu kiuchumi ili tuendelee kuwatia moyo na pia kuwapa fursa ya kutumia ujasiri wao katika kulinda nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo suala zima la mavazi yanayofanana na jeshi, wapo baadhi ya wananchi ambao wanatumia mavazi haya lakini kuna wananchi ambao wamenunua kihalali dukani wanayavaa, lakini wanapata bughudha na saa nyingine kudhalilishwa kutokana na mavazi yale. Niombe Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa basi atueleze ni kwa nini basi nguo zile zisipigwe marufuku ili wafanyabiashara wasipate hasara na wananchi wasiendelee kubughudhiwa kwa kuvaa mavazi yanayofanana na mavazi ya jeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la malalamiko katika maeneo mbalimbali ambayo yamechukuliwa na jeshi. Nikitolea mfano katika eneo la Mapinga Wilayani Bagamoyo, kuna maeneo ambayo Wanajeshi wamechukua, lakini hawajalipa fidia hadi sasa na wengine tathmini yao haikuwa nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu ana heka nne lakini anaandikiwa ana heka mbili, lakini mwingine anapiga tathmini bila kuangalia mazao yaliyopo ndani ya shamba lile. Mheshimiwa Waziri kwa kuwa na hilo pia analifahamu atakapokuja tunaomba tupate maelezo ni lini wananchi wa Mapinga Bagamoyo na maeneo mengine yenye tatizo kama hilo watalipwa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja aje pia na jibu ni lini Kambi za Jeshi zilizopo Mjini zitaondoka ili kuondoa bughudha kwa wananchi. Kumekuwa na changamoto nyingi katika maeneo ambayo Kambi za Jeshi zipo Mjini, nikitolea mfano katika Kata ya Majohe, Jimbo la Ukonga Mkoa wa Dar es Salaam ambapo Wanajeshi mara kwa mara wanavurugana na wananchi kwa sababu binafsi zikiwepo mambo ya mapenzi na ulevi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia Wanajeshi wetu wale wenye nidhamu nzuri wanaendelea kuonesha nidhamu nzuri na wanashiriki vya kutosha katika shughuli mbalimbali za dharura zinazojitokeza hapa nchini, yakiwepo mafuriko, matetemeko ya ardhi, lakini pia na ajali mbalimbali wanajeshi wamekuwa wa kwanza kujitokeza na kutoa msaada kwa wananchi, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina budi pia kutaka maelezo ya kina kuhusiana na maendeleo ya michezo ya Majeshi hapa nchini. Siku za nyuma Wanajeshi wengi walikuwa wanatupa sifa nchini katika michezo mbalimbali na hivyo kuitangaza Tanzania, lakini sasa hivi tumeona kimya. Je michezo Jeshini imekwisha au Wanajeshi sasa hivi hadhi yao kwenye michezo imeshuka? Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atueleze maendeleo ya michezo katika Jeshi yakoje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo niwapongeze wanajeshi hao na timu nzima kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuendeleza mila na desturi za Watanzania kupitia ngoma, michezo, sarakani na maigizo. Tumewaona kwenye shughuli mbalimbali za Kiserikali Wanajeshi hawa unawasahau kama hawa ni Wanajeshi jinsi wanavyoweza kuweka burudani na kudumisha mila na desturi za Kitanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa katika ajira tuangalie wilaya na mikao yote wapate ajira ili zile mila na desturi zinazolindwa jeshini ziwe za makabila yote, zisionekane ni za makabila mawili au matatu tu ndiyo yenye uwezo wa kutunza mila hizo kupitia jeshini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi katika suala la amani, wenzangu wengine walichangia lakini kuna mchangiaji mmoja ambaye alisema Tanzania sasa hivi haiko salama. Nataka kusema kwamba, Tanzania ipo salama ndiyo maana mpaka sasa hivi tupo hapa Bungeni. Wanajeshi hawa wamefanya kazi nzuri sana ya kulinda nchi yetu, kuna nchi wanalala saa tisa alasiri kwa sababu hakuna amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuonesha kwamba Tanzania amani ipo, bado tuna wimbi la watu wanaomba uraia wa Tanzania, kuna wimbi la watu ambao wanatoroka kwao wanataka kuja Tanzania, kuna maharamia haramu wamenga’ang’ania kuja Tanzania. Sisi tupo hapa unatoka Biharamulo mpaka Pemba, unatoka Mtwara mpaka Chato, unatoka Mbeya mpaka Chanjamjawiri, hakuna anayekuuliza hamna nini, halafu unasema Tanzania haina amani. Kipindi hiki ni kipindi cha kuwapa nguvu Wanajeshi wetu, kuwapongeza na kuthamini kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara hii bajeti yake isipunguzwe, wapewe kama walivyoomba na naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunisikiliza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais, lakini pia nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya Wizara hii kwa kazi nzuri wanazozifanya katika sekta ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi za Waziri pamoja na timu yake yote, nichukue nafasi hii pia kutoa pongezi kwa Taifa Stars, Serengeti Boys, Simba Sports Club, Chimo Olympic Maalum, Mabondia na timu ya Bunge Sports kwa kutuwakilisha vyema katika mashindano mbalimbali yaliyofanyika nje ya nchi. Aidha, nichukie nafasi hii pia kuwapongeza Wabunge wote Wawakilishi wote na Madiwani wote ambao wamekuwa wakiendeleza michezo katika maeneo yao kwa gharama zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Taasisi ya Sanaa Bagamoyo na Chuo cha Michezo Malya, wanafanya kazi nzuri sana, naomba Wizara isisite kuwapa fedha za kutosha ili waweze kutimiza wajibu wao na kuleta tija kwa malengo yaliyokusudiwa. Sasa hivi tunawasifia wasanii wetu na wanamichezo, lakini wengi wao hawajapita kwenye vyuo, ni vizuri basi vyuo hivyo vitumike vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii pia kuipongeza Taasisi ya Tulia kwa kuanzisha tamasha la ngoma za asili kila mwaka ambapo wameweza kutuletea burudani, kudumisha utamaduni lakini pia kutoa ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, msichoke kwa pongezi zangu, niwapongeze pia wasanii wote kwa ujumla. Naomba wasanii wadogo wawe wanaungwa mkono, wengi wao wana kazi nzuri, lakini wanashindwa kutuletea kwa sababu hawana fedha, aidha za kurekodi au kuziendeleza. Sasa ningefikiria itakuwa jambo zuri kama na wao wangeingizwa katika lile kundi la wajasiriamali ili wale wasanii wadogo waweze kurekodi kazi zao na kuweza kutuwasilishia.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mavazi kwa wasanii wanawake bado halijakaa sawa. Wasanii wanaume bado wanavaa vizuri, wanapendeza lakini wanawake, naona mpaka labda vitu fulani fulani vionekane ndiyo wanaona ngoma inanoga. Hata hivyo, nimpongeze dadayangu Vicky Kamata na dada mmoja anaitwa Siza Mazongela au mama Segere, wanaimba, wanacheza lakini bado wako katika mavazi mazuri ya heshima na wanapendeza. Kwa hiyo, naomba Wizara iendelee kulifanyia kazi suala la mavazi ya wasanii wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niombe wasanii hao wajitahidi sana kutumia ala za asili katika nyimbo zao. Kwa sababu, hasa wasanii wa kizazi kipya, wamekuwa wakitumia sana kompyuta, wakishatengeneza ile mistari yao wanakwenda kwenye kompyuta, sasa unaweza ukamkuta mwimbaji hata ukimpa gitaa, hawezi kutumia. Sasa ni vizuri basi wasanii wetu wawe wanatumia pia na ala za asili na wajitahidi kwenda katika chuo chetu cha sanaa ili waweze kupata mafunzo zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la filamu, filamu zetu wasanii wetu wanakwenda vizuri. Kuna tatizo moja katika zile scripts, niseme yale maneno ambayo yanapita chini pale wakati picha inaendelea kuangaliwa. Maneno yale naona mengi hayajahakikiwa vizuri, kuna Kiingereza kinachotumika pale nafikiri bado hakijakaa sawa. Aidha spellings zimekosewa na matokeo yake yanapoteza maana kabisa, ni vizuri basi ziwe zinapitiwa na kuangaliwa vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika vyombo vya habari, niwashukuru wana habari wote, wanafanya kazi nzuri na wanajitahidi kutuletea habari nzuri na zile mbaya tusizozipenda zote tunazipata. Tunawashukuru sana, lakini sasa kuna suala zima la vijana wabunifu ambao wametengeneza blogs zao na wengine wako online TV, lakini masuala ya usajili, ada na nini gharama imekuwa kubwa, kwa hiyo, ubunifu wao wanashindwa kuendelea nao wamekaa nao. Tuangalie jinsi gani tunaweza tukawasaidia ili tupate vyombo vingine zaidi vya habari vya kutufanyia kazi na kutupa taarifa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la utamaduni, tusiangalie tu ngoma, tuna suala pia la lugha. Katika suala la lugha matumizi sahihi ya lugha yetu ya Kiswahili ni mazuri zaidi na hili tulichukue hata huku Bungeni, unapomwona Mbunge ambaye ni mzazi na mwenye hadhi ya kitaifa anatamka maneno ya ajabu ajabu ndani ya Bunge, basi ujue huko nyumbani kwake ngoma kubwa. Hii inabidi tujirekebishe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TBC naomba iboreshwe, kama TBC Taifa, kuna wakati inatukwaza, tunasema hebu twende kwanza kwenye TV hii tuangalie, lakini inafika katikati, picha imeganda, ukienda kwenye television nyingine, picha inaendelea. Utakuta saa nyingine hotuba nzuri inayotolewa pale, unataka usikilize hotuba, maneno yameganda. Kwa hiyo, naomba,TBC ifanyiwe marekebisho ya kweli ili tunaposema hii TBC Taifa, iwe TBC Taifa kweli. Marekebisho yanafanywa, lakini sijaona bado, naomba…..

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Malembeka kuna taarifa!

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kumpa taarifa kwamba, kuganda kwa picha katika Shirika la Utangazaji la TBC ni kutokana na ubovu wa baadhi ya mitambo, vifaa vingi vimechakaa. Kwa hiyo, siyo tatizo kwa TBC bali ni umuhimu kwamba tuweze kutetea ili fedha zaidi ziweze kwenda TBC. Ahsante.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Amina Mollel, nilifikiri hiyo ndiyo hoja yake, kwamba TBC iweze kupelekewa vifaa. (Makofi)

Mheshimiwa Malembeka unaipokea taarifa hiyo!

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, huyo ni pacha wangu, kwa hiyo, nikiongea na yeye akichangia si mbaya, lakini neno kuboreshwa lina maana sahihi kama alivyozungumza, labda kama anataka uchambuzi tuanze kutoa mojamoja, kitu gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati nazungumzia hoja yangu ya kuboresha TBC Taifa, pia nishukuru Azam TV kwa channel yake ya Sinema Zetu. Imejitahidi sana kuwachukua wasanii hasa wadogo, tumewaona tulikuwa hatuwajui, tunaangalia picha zile zina maadili mazuri, waendelee hivyo hivyo. Halafu, huo mkakati wao wa kuwasaidia wasanii, basi uende vizuri ili wasanii waweze kupata haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dakika zangu ni kumi, muda ni mchache, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na huu ndiyo utekelezaji wa Ilani ya CCM. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia katika Wizara hii. Niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara hii pamoja na Taasisi zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukurani hizo, nitoe pia shukurani za pekee kwa Mheshimiwa Rais kwa kutimiza azma yake ya elimu bure kwa shule za awali mpaka sekondari, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu imeweza kuwekeza katika elimu maalum katika shule nyingi katika nchi hii, karibu Mikoa yote ina vyuo vya kutolea elimu maalum, isipokuwa Mikoa mitatu ambayo ni Simiyu, Geita na Songwe, nafikiri kwa sababu ni mikoa mipya ni vizuri Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuambie ni lini shule hizo zitafunguliwa katika mikoa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shule hizo, nilitaka nichangie kuhusiana na mashine au vifaa vinavyotumiwa na walemavu. Tumekuwa tunazungumzia suala la masomo yao, vitendea kazi vyao lakini hatujazungumza kwa kina vifaa vyao wanavyotendea kazi au vinavyowasaidia. Mpaka sasa hivi, tuna mafundi 65 tu ambao wanashughulika na mashine za walemavu, kati ya hao sita tu ni wanawake na 59 ni wanaume. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na idadi hiyo, fundi mtalaam mshauri, tunaye mmoja tu, ambaye yeye anafanya kazi Afrika Mashariki, Afrika ya Kati na Kusini mwa Afrika, ndugu Malim Kali, ambaye yuko pale Wizara ya Elimu, na msaidizi wake kidogo aliyekuwa anakuja kwa mbali, niseme kwamba Mwenyezi Mungu amuweke mahali pema, alifariki mwezi wa tatu mwaka huu!

WABUNGE FULAN: Ooooh!

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo, mafundi waliokuwepo, wana mafuzo tu ya awali na wengine wamepata vyeti, hatuna walimu tena, au mafundi wa kutengeneza zile mashine. Sasa Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa, nataka aje aniambie, wana mpango gani angalu wa kutengeneza program maalum kwa ajili ya mafundi wa kutengeneza mashine za walemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, yule fundi aliyekuwa mtaalam mkuu, aliyekuwa anatengeneza mashine za viziwi, naye amestaafu, bwana Robert Lugeiyamu, amestaafu mwezi Machi, mwaka huu, ni vizuri basi Waziri atakapokuja atuambie katika walataam hao wa kutengeneza mashine hao wamejipanga vipi ili walemavu waendelee kupata huduma zao pale vifaa vyao vinapoharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta hii ya elimu maalum, wamekuwa na ushirikiano mzuri sana baina ya Tanzania Bara na Visiwani, wamekuwa wakifanya kazi kwa pamojo na kwa ushirikiano mkubwa. Ni mara nyingi utakuta mafundi kutoka bara wanakweda Zanzibar na wengine wa Zanzibar wanakuja Dar es Salaam au Mikoa mingine ya huku kuja kujifunza au kufanya kazi. Sasa nilitaka kujua, ni lini mafundi hao watapata mafunzo, nchi nzima, bila kujali huyu Mzanzibar, au huyu Mbara ili waweze kuwatumikia walemavu katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna hizo shule kwa Pemba, tunazo tatu, Michakaweni, Mchangamdogo na Chakechake. Kwa Unguja, kuna Moga, Umoja, Uzini, Jambiani, Suza, Haile Selassie, CCK na Kisiwa Nduwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dar es Salaam, tunazo tatu, Uhuru Mchanganyiko, Msasani na Kibasila. Pwani ziko mbili, Lugoba Sekondari na Mwambao Primary, ambayo iko Bagamoyo. Tunayo Morogoro, Kilosa Sekondari na Mazimbu Primary, kwa Dodoma ziko nyingi kidogo, Mpwapwa TC, Mpwapwa Sekondari, Mvumi DCT, tuna Homboro Primary na Buigiri Primary Maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanga tunazo, Lushoto Maalum, Kongwe na Korogwe Grills, kwa Kilimanjaro tunayo Same, tunayo Mweleni, tunayo Moshi Technical na Saint Francis, lakini tunapokuja Arusha bado tunayo Temi, Patandi TC, Patandi Mazoezi, Lungido Primary na Longido Sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Manyara tuna moja, Kateshi Primary, lakini bado Mwanza, tuna Misungwi, Ukerewe, Kagera iko moja, Mugeza, ambayo iko Bukoba, lakini pamoja na hayo, Kigoma, wanayo Kabanga TC na Kabanga Primary. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haijajinyima, tukaenda Tabora tukakuta Furaha Primary, Shinyanga iko buhangija na Shy-Bush, ambako kuna Shinyanga Sekondary, Singida kuna Ikungi, kuna Singida Sekondari na kuna Kizega Primary. Kwa Iringa ipo Lugalo, ipo Makalale na Njombe kuna Mundindi Primary, hizo zote kwa ajili ya elimu maalumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbeya tunayo Katumba Two, Katavi tunayo Azimio Primary, Rukwa tunayo Malangale Primary, Kantaramba pia, lakini Ruvuma tunayo Ruhilo Primary, Ruhilo Sekondary, Songea Boys na Songea Girls. Kwa Lindi tunayop Nyangao Primary, lakini pia na Masasi Primary na Ndanda ikafutwa! Waziri anapokuja atuambie, kwa nini Ndanda waliifuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo nimeeleza mwanzo, Simiyu hakuna, Geita hakuna, Songwe hakuna, Je, wale walemavu wa kule tunawapeleka wapi kusoma, ni vizuri basi Serikali ijipange na ituambie lini itapeleka shule maalum katika maeneo hayo. (Makofi)

Pia nizungumzie kiwanda cha uchapaji kilichopo chini ya Wizara ya Elimu na Taasisi zake (Press A na Press B). Press A niwapongeze sana, wamefanya kazi nzuri katika mazingira magumo, vitabu hivi haa Wizara ya Elimu, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Habari na Utamaduni vyote wamechapa wao. Mashine za kizamani, kazi ya kumaliza siku moja siku nyingine wanafanya siku mbili au tatu, siku nyingine wanalala huko huko, basi Waziri akija atuambie mashine zile wana mpango nazo gani, sambamba na mashine za uchapaji za Press B kwa ajili ya wasioona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, nizungumzie kidgo kihusiana na suala lauwekaji wa viwango kwa walimu, viwango vya ushindishaji. Nafikiria labda viwango hivi wanaviangalia kwa watanzania, kuna baadhi ya shule za binafsi, walimu hao wapo wanaojiita walimu, lakini hawana sifa za ualimu, wanafikiria kuongea kingereza ndiyo sifa ya kuwa mwalimu. Tumefika baadhi ya shule tumeenda, tunakuta mtu, tena wanatoka nchi jirani, mwingine hana kibali cha kukaa nchini, mwingine hana kibali cha kufanyia kazi, hana sifa yoyote ya ualimu, lakini amepewa hiyo kazi, ninaomba mpite kwenye hizo shule mkakague. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati huohuo nitoe pongezi zangu za dhati kwa wamiliki na wenye shule wote wa private, ambao wamekuwa watiifu na wanafanya kazi vizuri, kuisaidia Serikali kuboresha elimu katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo mengi mazuri yamefanywa katika Wizara hii ya Elimu, lakini kuna madogomadogo ambayo yameguswa inabidi yafanyiwe kazi na kuwekwa sawa. Katika mambo hayo, kuna masuala ya rushwa ya ngono katika vyuo na vyuo vikuu yametajwa, kuna masuala ya wizi wa mitihani, kuna masuala ya upendeleo katika usajili wa vyuo uliopelekea kusajili vyuo ambavyo havina sifa na hatimaye kuwapa wanachuo shida ya kuacha shule mapema au kuondolewa, halafu chuo kinafungwa, wanapata tabu, ni vizuri watuambie, wamejipanga vipi kudhibiti hali hiyo ya rushwa kwenye vyuo, upendeleo kwenye usajili na wizi wa mitihani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kabla sijamaliza, bado kuna suala lingine la kuzungumzia kuhusiana na elimu kwa redio…

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja asilimia mia kwa mia, na mwisho nasema siasa kwenye chama zinaendelea kwa sababu tunaanza chini tunakwenda juu, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye Wizara hii. Kwanza namshukuru Mwenyenzi Mungu kwa kuniamsha salama. Nitoe pongezi kwa Amiri Jeshi Mkuu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Joseph Pombe Magufuli kwa kuiongoza nchi yetu vizuri na kazi nzuri anazo zifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nichukue fursa hii kumpongeza Waziri mwenye dhamana kwa kazi nzuri, zenye tija zinazoendelea kufanywa kwenye Wizara yake, pongezi hizi pia ziende pia sambamba kwa makamanda na Maafande wote nchi bila kuwasahau watendaji wao katika nafasi zao. Kipekee napenda kuwapongeza vijana wote wanaojitolea katika Jeshi la Kujenga Taifa tunawatambua, tunathamini mchango wao na tunawajali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania nasema ni salama na usalama huu unatokana baina ushirikiano baina ya Wizara hii, Wizara nyingine pamoja na wananchi na pia niwakumbushe wananchi kwamba usalama wa nchi ni jukumu letu sote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunao vijana wengi ambao bado hawajapa ajira japo wamekuwa wakijitolea katika vituo vya JKT hapa nchini. Ninaomba Serikali iangalie upya jinsi gani wataweze kuwa ajiri vijana hao. Lakini pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais ambaye
aliweza kuruhusu ajira zitolewe kwa vijana waliojenga ukuta wa Marerani na waliojenga Mji wa Seriakali hapa Dodoma. Lakini Waziri atakapokuja atuambie Wizara yake imejipangaje kwa ajili ya kutoa ajira kwa vijana hao badala ya kusubiri matamko ya Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia SUMA JKT kwa kazi nzuri wanazifanya. Wamekuwa wakifanya kazi nzuri na zenye uhakika na gharama naafuu naomba tuenelee kuwaamini na kuwapa kazi ambazo zinaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi letu limekuwa na ushirikiano mzuri na majeshi mengine katika nchi nyingine katika masuala ya ulinzi na amani na usalama kwa ujumla wake, katika kuboresha maslahi ya watendaji katika vyombo vya ulinzi na usalama ningependa kujua kwa jumla Mheshimiwa Waziri wiki nzima hii tumekuwa na clip au taarifa ambazo zinatembea kwenye mitandao zikionesha baadhi ya Watanzania na wananchi wa nchi jirani ambao wanasema kwamba wamepigwa Afrika Kusini au wamechomwa moto. Sasa Waziri angetuambia taarifa hizi ni za kweli au ni mitandao tu na kama ni kweli Waziri anatueleza nini kuhusiana na hilo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa suala la ulinzi na usalama limo katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2025 na pia limo katika Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa miaka mitano, 2016/2017 mpaka 2020/2021 na utekelezaji wa majukumu mengine katika Wizara hii, mimi naomba niwashawishi Wabunge wenzangu tukubali na kuipitisha bajeti ya Wizara hii ili waweze kuweka mazingira mazuri ya JKT na kuimarisha mafunzo ya vijana, pia kushirikiana na Umoja wa Mataifa (UN) na Umoja wa Afrika katika shughuli za ulinzi na amani. Pia waweze kushirikiana na mataifa mengine katika kupambana na uhalifu unaovuka mipaka ikiwepo ugaidi, uharamia na biashara haramu ya madawa ya kulevya. Lakini pia kuviwezesha vyombo vya ulinzi na usalama kuviongezea rasilimaliwatu na fedha ili waweze kufanya kazi zao vizuri. Sambamba na hilo kufanya tafiti mbalimbali zenye maslahi kwa wanajeshi na raia kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuunga mkono maombi ya bajeti kwa ajili ya Wizara hii, ninaomba Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake atueleze ni lini Serikali italipa fidia au kurejesha maeneo ambayo wanajeshi walichukua kutoka kwa raia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi pia limeweza kuwekeza katika maeneo mbalimbali, lakini katika uwekezaji wake ni vizuri aje atueleze ni utaratibu gani unaotumika unaotumika katika uwekezaji unaofanywa na Jeshi bila kuzingatia mipango miji na haiba ya mji. Nikitolea mfano Jimbo la Welezo eneo la Jeshi kuna biashara pale za gereji, za kuuza miti, kuuza vyakula, kuosha magari wote katika eneo moja. Naomba Mheshimiwa Waziri akija atueleze vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo jeshi limekuwa na kumbi mbalimbali za burudani, nilitegemea kumbi zile zitatumika zaidi na wanajeshi. Sasa hivi kumbi zile zimekuwa zinaingiliwa na raia wa kawaida pamoja na wanajeshi na katika burudani zile mara nyingi ugomvi unatokea na ugomvi huo mara nyingi unahusishwa na pombe pamoja na wanawake na katika vita hivyo siku zote wanaopigwa ni raia wanajeshi wanakuwa ndio washindi. Sasa tunataka watuambie ni lini au ana tamko gani kuhusiana na maeneo hayo ya burudani ili wananchi wetu wasiendelee kupigwa, aidha kutokana na masuala ya pombe au masuala ya mapenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia vituo vya afya vinavyioendeshwa na Jeshi nikitolea mfano Kituo cha Bububu - Zanzibar, Kituo cha Welezo - Zanzibar, Lugalo - Dar es Salaam pamoja na vituo vingine. Vituo hivi vimekuwa vinafanya kazi nzuri sana na wananchi wanapenda sana kwenda kutibiwa pale kwa sababu kwenye vituo vile wanajali sana wagonjwa, wanatoa huduma nzuri na wana upendo wa dhati, lakini tatizo kubwa pale ni bajeti finyu, wanakuwa na bajeti ndogo ambayo wanashindwa kuwa na dawa za kutosha japo wanatoa huduma nzuri. Ni vizuri basi Serikali waviangalie vituo hivi kwa jicho la huruma ili wananchji waendelee kupata huduma na nikiamini kwamba Jeshi liotaendelea kuisaidia Serikali katika kutoa huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze tena wanajeshi wetu wote kwa kazi nzuri za ulinzi na usalama zinazofanyika hapa nchini. Maneno madogo madogo yapo, lakini hayo Jeshi wakiamua kunyamaza humu ndani hakukaliki tusidanganyane. Jeshi linafanya kazi nzuri sana na katika 100 mtu akikosea 10 akapata 90 maana yake ndio kashinda kafanya vizuri. Lakini kipekee niwapongeze...

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu mwenye wingi wa rehema alotuwezesha Wabunge sisi wote mpaka leo hii kuwepo hapa kujadili haya ambayo tunayazungumza.

Nitoe pongezi kwa Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya yeye na timu yake yote Mawaziri, Makatibu Wakuu na watendaji wote kwa ujumla. Lakini kipekee nimpongeze Mheshimiwa Jafo kama yeye hongera sana Mheshimiwa Jafo umefanyakazi nzuri kwenye Wizara yako wewe na wasaidizi wako lakini kazi hii hujaifanya tu vizuri kwenye nchi, lakini pia umeifanya vizuri katika Jimbo lako Mwenyezi Mungu atakusaidia utarudi tena In Shaa Allah.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe pia pongezi zangu kwa Makamu wa Rais mama Samia Suluhu, kwa Waziri Mkuu, kwa Rais wa Zanzibar, Makamu wa pili wa Rais Zanzibar kwa jinsi wanavyoweza kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi na kuweza kutufanya Wabunge wa Chama cha Mapinduzi tusimame tukijidai kwamba kazi imetekelezeka. Kipekee pia niwashukuru na niwapongeze Wabunge wote ambao Awamu zote Nne walikuwa wanasema ndiyo ili kazi ifanyike na ninaomba mwaka huu tusisite tena tupige ndiyo ili kazi iliyobaki ikamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuchangia kuhusiana na suala zima la uwezeshaji kiuchumi wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kupitia asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri hadi sasa hivi bilioni 93.3 zimekopeshwa bila riba kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Vikundi 915 vya watu wenye ulamavu vikundi 4266 vya vijana na vikundi 8207 vimepata mikopo hiyo hapo ninachoomba wale waliokopeshwa warudishe lakini hapo hapo halmashauri ziendelee kutoa mikopo hii kwa wananchi kwa sababu hii ni ahadi iliyotolewa na Chama cha Mapinduzi ni lazima itekelezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia ujenzi wa majengo ya utawala majengo ya utawala yamejengwa 86 kati ya hayo 29 yamekamilika na 57 yako katika hatua za mwisho za kukamilika ili Wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa wakae katika maeneo mazuri. Niipongeze sana Serikali yangu kwa kujali watumishi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wameeleze katika sekta ya elimu madarasa 19,808 yamekamilika, napenda niongezee kwamba madarasa 1313 yanaendelea yako katika ujenzi yatakamilika wakati wowote. Lakini kuna maabara 227 zimejengwa nipende tu kuongezea kwamba katika maabara hizo vifaa vya maabara vimeshatolewa katika sekondari 1258 ni jambo zuri sana ambalo Serikali imelifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la matundu ya vyoo ambalo 7922 yamekamilika na mengine 571 yako katika ujenzi na yako katika hatua za mwisho ambazo wanategemea kukamilisha muda si mrefu. Shule kongwe zimetajwa 73 zimekarabatiwa vizuri lakini nilizungumzia masuala ya mabweni mabweni yamekarabatiwa kiasi kwamba yanaonekana ni mapya ile ni kazi nzuri sana ambayo imeonyesha jinsi gani TAMISEMI imeweza kuokoa kwa sababu bila kukarabati yale majengo yangeharibika kabisa na tungepata hasara mpya ya kujenga majengo mapya. (Makofi)

Suala la hospitali zimeelezewa hapo hospitali 98 kuna vituo vya afya kadhaa kuna zahanati kadhaa mchango wangu hapa nilitaka niongeze kwamba Chama Cha Mapinduzi kupitia utekelezaji wa Ilani imeweza kuwezesha upatikanaji wa dawa na vifaa vya tiba kwa 92% hayo ni maendeleo makubwa sana. Lakini kwa kuwa kuna watu ambao roho zao hazina sifa za kusifia hatuwezi kuwalaumu lakini mwenye macho anaona mwenye masikio anasikia na wengine ndiyo huko huko wanaenda kujifungua wanaona zile hospitali wengine ndiyo huko huko watoto wao wanasoma lakini wanashindwa kusifia sisi tumuombe Mwenyezi Mungu tu amuwezeshe Rais wetu na Mawaziri wake wafanye kazi vizuri Mwenyezi Mungu uko pamoja nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la corona suala la corona limekuja ghafla na kwa kazi kwenye suala hili nimpongeze Waziri wa Afya na timu yake pamoja na Waziri Mkuu lakini pia kipekee niwapongeze watumishi wote wa sekta ya afya popote nchini. Kwa sababu kila mtu anaogopa kufa lakini wale wenzetu inabidi watoke waende kule kuhudumia watu ninawapongeza sana sana sana na ninaomba tufate maelekezo ya wauguzi, madaktari na viongozi wetu. Kwa mfano hapa Ofisi ya Bunge tumejitahidi sana kujilinda kwa namna yoyote lakini je hivi tunavyojilinda tukitoka nje ya Bunge na sisi tunaendelea kujilinda? Kule Chako ni chako tunaacha kwenda? Huku na huku tunaacha kwenda? Naomba hilo tuliangalie kwasababu vinginevyo tutakuwa tunatunzwa vizuri hapa Bungeni halafu tukitoka nje tunabeba ya kule nje tunaleta humu Bungeni inakuwa sawa sawa na bure. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine pia huko kwa wananchi wetu tusaidiane pia kuendelea kutoa elimu isije ikaonekana sisi huku tunatunzwa halafu wananchi wetu wanapata tatu. Kwa hiyo, Wabunge tukitoka hapa tukirudi na sisi tuwajibike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine tusaidiane na Serikali kwa sababu hili suala lilikuwa haliko kwenye bajeti Mbunge ambaye anaweza kujitolea kwa ajili ya kusaidia visafisha mikono na vitu vingine aendelee kutoa ili muda ukipita basi tujue na Wabunge nao tuliwajibika isije ikawa hapa 90% tunawasema tu Mawaziri, sijui nani hawajafanya nini, je sisi kama Wabunge tumefanya nini? Hilo nalo tujipime na sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka wa uchaguzi dakika za mwisho tusitafutiane fitna na maneno yapo maneno ya kuudhi ambayo yanatugusa sisi wengine hatupendi kuyasema tuombeane dua. Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa ina wajumbe kutoka Zanzibar sita na wanazunguka nchi nzima kufanya kazi sasa mtu anaposema huku siyo Zanzibar hatuendi hivyo tufanye kazi na tuheshimiane.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa fursa ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa tarehe 13 Novemba, 2020.

Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kurudi tena katika jengo hili. Pia nakishukuru Chama change Cha Mapinduzi, Jumiya ya UWT, wapiga kura wangu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja na wote kwa namna moja au nyingine walioshiriki kunifikisha katika jengo hili, ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natoa pongezi pia kwa Mheshimiwa Rais wa Tanzania, Mheshimiwa John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais Mama Samia na Waziri Mkuu Mheshimiwa Majaliwa. Pongezi hizi hazitatimia kama sitaweza kutoa pongezi kwa Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Mwinyi pamoja na Makamu wa Kwanza wa Rais na Makamu wa Pili wa Rais ninawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hotuba zote mbili nilizisikia na nilizisoma kwenye vitabu. Nitachangia kwa machache nikianza kwanza kwa kuungana na wenzangu kuunga mkono asilimia mia moja hotuba hii. Pia niseme kwamba wengi wanatuambia tunapenda sana kupongeza, niseme tu tunapongeza kwa sababu vya kupongeza vipo, kama hakuna vya kupongeza hatutapongeza, tunaendelea kupongeza kwa sababu vya kupongeza vipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ukurasa wa tatu na wa nne ameelezea juu ya Tume ya Uchaguzi ilivyofanya vizuri. Mimi naunga mkono na niwapongee sana, kitendo alichokifanya ni sawasawa na mtende kuota jangwani, kati ya shilingi bilioni 331 wameweza kutumia shilingi bilioni 262 na kubakiza shilingi bilioni 69 hayo ni maajabu. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Kiruswa umevunja utaratibu, umepita kati yangu na mzungumzaji, kwa hiyo, rudi ulikotoka. Kwa Wabunge wageni Mbunge yeyote anayeongea unaacha line yake na Spika huruhusiwi kuikatiza. Endelea Angelina Malembeka.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, naomba nitunziwe muda wangu. Ninaendelea kusema kwamba naipongeza Tume ya Uchaguzi kwa kazi nzuri waliyoifanya kwa kutumia shilingi bilioni 262 kati ya shilingi bilioni 331 na kubakiza shilingi bilioni 69, nimesema hayo ni maajabu ya mtende kuota jangwani. Hii imeonesha uadilifu mkubwa kwa watumishi wa umma na imeonesha jinsi gani nidhamu sasa ilivyotapakaa, ninaomba hali hii iendelee katika siku zijazo tusisifie sasa halafu baadae mambo yakawa yamebadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ukurasa wa saba Mheshimiwa Rais alielezea jinsi gani ambavyo atatoa ushirikiano wa kutosha kwa Rais wa Zanzibar. Suala hilo sisi tumelifurahia sana kwa sababu wakati hata anaomba kura Zanzibar alisema niletee Dkt. Mwinyi nitawasaidia, nitawanyanyua uchumi wa Zanzibar na sasa hivi tuko katika Zanzibar upya, uchumi mpya tunategemea haya aliyoyasema atayatekeleza na tunamuombea kila la kheri ayatekeleze ili Zanzibar ibadilike kama ilivyopangwa.

Mheshimiwa Spika, katika ukurasa wake wa 11 alielezea mifuko mbalimbali na programu ambazo zimeanzishwa ili kusaidia wananchi ikiwepo Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake, Mfuko wa Taifa wa Kuendesha Wajasiriamali, Mfuko wa Kutoa Mikopo, lakini katika mifuko hiyo hakuna mfuko wa wavuvi wadogo wadogo.

Nilikuwa ninaomba basi uanzishwe mfuko kwa ajili ya wavuvi wadogo wadogo waweze kukopa wao kwa riba nafuu au mkopo usio na riba ili waweze kununua vifaa vya kisasa vya uvuvi ambavyo vitasaidia pia kuondoa uvuvi haramu katika bahari zetu na tukiangalia sasa hivi tunaingia katika uvuvi wa bahari kuu na uchumi wa blue ambapo tunategemea kwamba meli kubwa za kisasa zinanunuliwa ziweze kufanyakazi. (Makofi)

Lakini kama tutanunua meli kubwa za kisasa, lakini bado wavuvi wadogo wadogo wanaendelea kutumia mabomu kuvua bado tutakuwa hatujafanya kazi. Kwa hiyo niombe kwamba mfuko maalum uandaliwe kwaajili ya wavuvi wadogo wadogo waweze kukopeshwa.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo uwekezaji katika sekta ya uvuvi basi wale wawekezaji wazawa nao wapunguziwe kodi ili waweze kuleta samaki wengi na wakileta samaki wengi samaki bei itashuka na kila mwananchi ataweza kula samaki na hivyo kuboresha afya zetu. Tukiwawekea kodi kubwa na meli za uvuvi zitakuwepo halafu samaki tutashindwa kununua, kwa hiyo nilikuwa naomba hilo pia liangaliwe.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo nimeona nilizungumzie ni kuhusiana na suala la Corona ambalo katika ukurasa wa 32 na 33 limezungumziwa. Tumeona umuhimu wa kutumia dawa tiba au mitishamba au dawa mbadala, hili suala kwa kweli nimshukuru Mheshimiwa Rais ametupa ujasiri ametupa nguvu tunasimama hatuhangaiki, sasa hivi hata mtu tukimuona anakohoa tunajua jinsi gani ya kufanya, lakini mwanzo ilikuwa hata ukiona jirani yako anakohoa unatafuta kiti cha kuhama umkimbie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sasa hivi tumepata ujasiri, tumeendelea kutumia hizo dawa lakini pia nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Jafo kwamba mzee wa nyungu tumepata nguvu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Angelina, tunakushukuru sana.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Ninaomba zile taasisi zinazoshughulika na utafiti pamoja na kutoa vibali kwaajili ya dawa hizo zifanye haraka ili dawa zisambae wananchi wapate huduma naunga mkono hoja ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini pia nichukue nafasi hiyo hiyo kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianzie na suala zima la utumishi kuhusiana na suala la uhamisho. Kumekuwa na tabia ya kuwaambia watumishi akatafute mtu wa kubadilishana naye. Kwa kweli kitendo kile mimi binafsi naona kwamba ni kumsumbua mtumishi lakini pia kumfanya asifanye kazi zake. Mtu yuko Mwanza anataka kwenda Mtwara anaambiwa akatafute mtu wa kubadilishana naye.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikichukulia mfano wa walimu ule muda ambao alitakiwa awe anafundisha inabidi atoke aende kwenye halmashauri kuangalia kama kuna mtu anayetaka kuja Mtwara na halmashauri nyingine zipo mbali na kituo cha mtumishi. Naomba Wizara iwe na mbinu mbadala, badala ya kumwambia mtumishi akamtafute mwenzie wa kubadilishana naye basi Wizara iangalie nani anataka kwenda Mtwara apelekwe na yule wa Mtwara anayetaka kwenda Mwanza apelekwe badala ya jukumu lile kumuachia mtumishi mwenye ahangaike nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine nizungumzie posho za Madiwani, imekuwa ni utaratibu kila Bunge tukija tunazungumzia posho za Madiwani. Wale ni wenzetu tunafanya nao kazi, tunapokuwa tunasema halafu hawatekelezewi tunaonekana pia Wabunge hatuna maana tuna ubaguzi. Naomba Wizara isimame kidete kushughulikia posho za Madiwani na ikiwezekana wawape mshahara maalum ijukane Diwani ana mshahara shilingi ngapi kwa mwezi halafu hizo posho aendelee kuchukua kutokana na vikao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nalisema hili kwa sababu kuna vikao vya Madiwani vinafanyika hawapewi hata hiyo posho yenyewe ya kikao, wanasema halmashauri haina fedha. Madiwani wanakopwa, wanakwenda kwenye vikao wengine wanatoka mbali nauli hawana, wanapata usumbufu lakini wapo chini zaidi kwa wananchi hata mwananchi akimwambia tunataka timu yetu ya kwenye mtaa tupate mpira fedha ya kununua mpira hana. Kwa nini tusiwafikirie Madiwani ili na wao waweze kufanya kazi zao kwa umakini zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala zima la uandikishaji wanafunzi wa darasa la kwanza. Halmashari nyingi zimeonesha kwamba zinaandikisha watoto wengi lakini ukifuatilia wanapofika mwisho ile idadi inapungua na inapungua kuanzia darasa la tano, la sita mpaka darasa la saba. Ukiangalia sababu kubwa ni utoro na mimba za utotoni au mimba zisizotarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niziombe basi halmashauri ziweke mkakati wa dhati kati ya halmashauri na wazazi kuhakikisha wale watoto wanaoandikishwa wafike shule na ikibidi kama kushtaki basi na mzazi naye ashtakiwe. Kuna wazazi wanaojua kabisa mtoto wangu haendi shule na yeye yupo kimya, kama elimu imetolewa bure kwa nini halmashauri ziandikishe watoto 600 halafu mwisho wa siku watoto wako 200 hao wengine wamekwenda wapi? Ni lazima tujizatiti kuhakikisha kwamba wanafunzi walioandikishwa wamalize kama ilivyotarajiwa badala ya kuwa na sifa kwamba tumeandikisha watoto kadhaa lakini mwisho wa mwaka tunajikuta watoto wako kidogo kwa sababu ya utoro na mimba zisizotarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilizungumzie suala la uwezeshaji kiuchumi kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Zipo halmashauri zilizofanya vizuri lakini kuna halmashauri zingine hazitoi zile asilimia 10, wanajipangia wanavyotaka wao. Ukiangalia makusanyo yao ya mapato ya ndani hayalingani na zile pesa wanazozitoa. Ni vizuri suala hili lisimamiwe ili zile asilimia 10 zitolewe kama zilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika utoaji wa asilimia hizi haki itendeke kuna vikundi ambavyo viko ndani ya halmashauri havijawahi kupata mikopo hii.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Boniphace Getere.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba hii kero ya asilimia 10 kwa halmashauri zote nchini Tanzania ili imalizike inatakiwa kuwepo na akaunti mbili benki; akaunti hiyo ya asilimia 10 na akaunti ya Halmashauri. Kila fedha ya halmashauri inayoingia kwenye akaunti ile asilimia 10 iende kwenye akaunti. Hilo ndiyo itakuwa suluhisho ya kero hii. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Getere huo ni ushauri kwa mchangiaji au ni taarifa kwa mchangiaji?

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Angelina Malembeka, malizia mchango wako.

MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Taarifa hiyo nimeipokea kwa mikono miwili kwa sababu inaleta tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mgao huo huo wa asilimia 10 napenda kuongezea kwamba utaratibu ufanyike. Kwa sababu kuna Halmashauri ambazo unakuta kuna kikundi kinapata mara mbili mpaka mara tatu lakini kikundi kingine mpaka miaka mitano inapita hawapati. Kama wanakosea kufanya utaratibu mwafuate, mwaeleze jinsi gani wafanye ili na wao wapate ile mikopo. Badala ya kuwa wanaomba miaka yote hawapati lakini makundi mengine yanapata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hilo, pia ni vizuri basi Halmashauri zijipange tuone zile fedha za marejesho zinazorudishwa, ziko wapi na zinafanya nini? Isiwe kila mwaka wanapanga shilingi milioni tano, mwaka unaofuatia milioni tano, mwaka unaofuatia milioni tano, lakini zile zinazorudishwa hazionekani ziko wapi na zinafanya nini? Ni vizuri zionyeshwe na tujue zinafanya nini; kama zinaongezwa kwenye mikopo au zinafanya kazi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia suala zima la ukarabati wa shule kongwe na baadhi ya Vyuo vya Ualimu. Kazi imefanyika nzuri sana, lakini hapa hoja yangu ni kwamba, tusiwe tunasubiri tu kukarabati shule kongwe na zile zilizopo ukarabati mdogo mdogo uwe unaendelea kufanyika ili kuondoa madhara makubwa. Kwa sababu unapokuta labda jengo limebomoka mlango mmoja, siyo tunasubiri mpaka milango yote ivunjike na madirisha yote yavunjike, haitaleta tija. Ni vizuri hizo shule ambazo bado ni mpya lakini zimeanza kuonesha matatizo zianze kukarabatiwa mapema ili kuondoa athari kubwa kwa siku za baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuzungumzia suala zima la ukamilishaji wa maboma ya majengo mbalimbali yaliyoanzishwa na wananchi. Wananchi waliitikia mwito wa kujitolea wakajenga nyumba mblimbali; kuna nyumba za walimu, zahanati, shule na vituo vya afya. Sasa yale maboma kwanza yanawatia uchungu wananchi. Wameacha shughuli zao ku-support Serikali halafu Serikali mpaka sasahivi wanayatazama. Ni vizuri tujipange ili yale majengo yaliyoanzishwa na wananchi yakamilike ili waweze kuyatumia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa ili niache fursa kwa wenzangu kuchangia, nizungumzie suala zima la mama wajawazito na watoto hususan kwenye vituo vya afya. Kuna maeneo ambayo wanasema huduma hii inatolewa bure, lakini ukienda unakuta huduma hizo zinalipiwa kwa njia ya ujanja ujanja. Mtoto ana tatizo hili, anaambiwa chukua karatasi nenda kanunue kitu fulani. Mtoto ana tatizo hili, nenda kanunue dawa fulani, wakati hizo dawa wakati mwingine zinapatikana kwenye lile eneo na wazee wanafanyiwa mambo hayo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri pia tujipange tuangalie jinsi gani ya kukamilisha hili zoezi bila kutia kero kwa wananchi kwa sababu kama tumekubaliana elimu bure, afya bure kwa wale ambao wana sifa za kupata wapate bure kweli. Siyo wanaenda pale wanalipishwa kumwona daktari na kadhalika, halafu na dawa zenyewe hawapati wanaambiwa wakanunue. Hiyo siiafiki, tujipange vizuri, Halmashauri zifanye kazi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na afya yangu, leo naomba niishie hapo. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami kuchangia katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Kwanza nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri sana wanayoifanya. Hii imeonyesha jinsi gani migogoro ya ardhi ilivyopungua hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi tunajua ni asilimia 25 tu ya ardhi yetu ambayo imepangwa na kupimwa. Kati ya hizo, kuna viwanja 2,337,938 ambavyo vimepangwa. Tuna miliki zilizotolewa 1,557,819; tuna vijiji vilivyopimwa 11,743,000 ambavyo vimepimwa na kuandaliwa hati ya ardhi; na pia tuna hati zilizosajiliwa 868,474. Hii ni dalili tosha kuonyesha kwamba kazi ndani ya Wizara hii inafanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 75 iliyobaki, nasema, kama Wizara imejipanga vizuri, lakini kuna watu au taasisi ambazo zinawarudisha nyuma. Kama wameweza kufanya kazi hii, naona kila mtu abebe mzigo wake mwenyewe, kwa sababu inafika sehemu mtu anafanya kazi lakini mwenzie anamrudisha nyuma. Yeye anashindwa kufanya kazi zake anamsababisha na mwingine ashindwe kufanya kazi. Hii ipo kwa baadhi ya Wakurugenzi wa Halmashauri. Wamepokea shilingi milioni 400 ili wapime hivi viwanja na kuvipanga vizuri, matokeo yake wamefanya vitu vitatu tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo kundi la kwanza ambao wamefanya vizuri, tunawapongeza. Kuna kundi la pili wamekwenda wamebadilisha matumizi kwa kuwasingizia Madiwani. Kuna kundi la tatu wamekamilisha ule mradi halafu wameanzisha mradi mwingine na pesa hawajarusdisha wakati wanajua kuna Halmashauri nyingine zinahitaji fedha hizi ili wapange miji yao vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wakurugenzi hawa ambao wamekiri, mimi nasema kwa sababu niko kwenye Kamati ya TAMISEMI, tumewaita na kuwahoji, wamekiri lakini wanatoa kisingizio cha Madiwani. Sasa naomba wasiwasingizie Madiwani. Wao ndio Watendaji Wakuu na ndio wataalam, kwa nini wasingizie Madiwani wamebadilisha matumizi? Kama kweli wanafuata utaratibu wa Madiwani, mbona Madiwani wakisema tunawafukuza Wakurugenzi, wanaanza kusoma kanuni, sheria na taratibu ili mradi wabaki? Kwa nini na huku wasitoe utaratibu? Kwa nini wasiwaongoze Madiwani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanafika sehemu agenda nyingi zinapokuja pale, mimi najua; kuna baadhi ya ajenda ambazo zinaletwa moja kwa moja na Madiwani, lakini kuna ajenda nyingine zinatoka kwenye Kamati ya Fedha na Utawala, wanakuja nazo pale kujadili; na wale ni wataalam tunategemea kwamba wataongea na Madiwani, watawaelimisha halafu Madiwani watafanya maamuzi. Ila wakishaona hii hoja ina maslahi kwao, basi wanawadanganya wale Madiwani ili mradi tu waseme ndiyo halafu waje waharibu. Katika hili Mkurugenzi mmoja, sina haja ya kumtaja jina au Halmashauri yake, anasema kabisa nimewasomesha Madiwani wakakubali, tumebadilisha matumizi; kwa sifa tu, wala hana wasiwasi wowote. Sasa kwa nini mwasingizie Madiwani?

Mheshimiwa Naibu Spika, itafika kipindi hapa akija Mkurugenzi tunamwambia njoo na Meya wako ili tuone ukweli uko wapi? Kwa sababu wale Mameya na wale Madiwani wenyewe hawapo huko ndiyo maana Wakurugenzi wengine wanasema sivyo. Kinachotakiwa sasa hivi, wale waliochukua shilingi milioni 400 za mkopo bila riba, warudishe ili wenzao waweze kufanya kazi katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mnasema Serikali na Serikali mnashindwa kushitakiana, mimi nasema kwenye hili Waziri amtafute Waziri mwenzake wa TAMISEMI awabane Wakurugenzi wake fedha zirudi. Kuna miji mizuri sasa hivi inashindwa kuendelea kwa sababu haijapangwa. Watu wanapewa fedha wanabadilisha matumizi. Kama hamzitaki, kwa nini mlizichukua? Nasema kabisa mpango huu ni kumvuta shati Waziri wa Ardhi na Naibu wake ili kazi isiendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu hii ardhi ni mali ya Halmashauri. Hawa Halmashauri ndiyo wanatakiwa wapange hapa kuna shule, hapa kuna zahanati, hapa kuna kiwanja cha michezo, hapa kuna soko, ni kazi ya Halmashauri. Cha ajabu wanapokaa kwenye bajeti zao hawapangi kwamba tunatenga kiasi hiki kwa ajili ya kupanga miji na kupima, wanasubiri mikopo ambayo hawataki kurudisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hili naomba Wakurugenzi ambao wamechukua fedha na hawajarudisha na pia wengine wamebadilisha matumizi, hatua za nidhamu zichukuliwe dhidi yao. Kwa sababu utawala bora ni pamoja na kuheshimu matumizi ya fedha na kuwa na nidhamu ya fedha na matumizi yake. Hatuwezi tukawa tunapitisha fedha halafu watu wanabadilisha matumizi, wengine wanakosa, yeye amekaa tu ame-relax anasingizia Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na taarifa hiyo, bado kuna suala lingine la ardhi ambalo wote mara nyingi tunalalamikia. Ndani ya Halmashauri mpangilio uko mzuri, kuanzia ngazi ya Halmashauri kwenye Kata, kwenye Vijiji mpaka kwenye Mitaa. Mtu anaanza kujenga wanamwona, anachimba msingi, anaweka tofali wanamwangalia, anapiga plasta wanamwona, anapiga bati wanamwona; akishahamia anaambiwa bomoa, hapa kuna barabara inapima. Hiyo mipango miji hamuioni? Kwa nini tuwatia hasara wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama utendaji upo na Maafisa Mipango Miji wapo, wakiona msingi umechimbwa, basi waende wakamwambie mapema hapa usijenge kuna barabara inapita, lakini siyo anamwacha amejenga mpaka mwisho, anamaliza, unamwambia abomoe, hela yenyewe ya kuungaunga, utabomoa mara ngapi? Sisi tunawajua Watanzania wenzetu. Pesa hatuna, kujenga kwenyewe kwa kudunduliza, kwa nini uningoje nipige bati ndiyo uniambie nibomoe? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba hawa watu wa Mipango Miji huko wazunguke kwenye mitaa yao, maeneo ambayo wanaona haya kuna kitu kingine kinakuja wasiruhusu watu kujenga, wawaondoe kabisa. Hii inatokana na huo uzembe wa hizo fedha, badala ya kwenda kuwapangia watu wapate viwanja halali wanawaacha wanazagaazagaa tu wanajenga popote. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mengi ya kuongea kuhusu Wizara hii lakini kwa leo naomba niishie hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia mada iliyoko mbele yetu. nichukue nafasi hii pia kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniweka hai hadi leo. Niwashukuru Wabunge Wote, Mheshimiwa Spika na Katibu wa Bunge kwa jinsi ambavyo mliweza kuniliwaza na kunihudumia nikiwa hospitali. Ninaendelea kuwashukuru Madaktari wote walionihudumia. Leo ni mara yangu ya kwanza kuchangia baada ya mwaka mmoja. Namshukuru Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza waziri kwa uwasilishaji mzuri, nimemsikiliza vizuri nampongeza yeye, Naibu wake na timu yake yote. Pia nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazozifanya nchini mwetu ambazo zimetuongezea sifa ndani ya nchi na nje ya nchi. Pia wanawake, vijana na watoto tumeona maendeleo ya wazi ambayo kila mtu bila hata ya kumuonesha anaona kwamba nchi imebadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la ukatili na unyanyasaji. Wengi tumekuwa tukizungumzia watoto,wanawake na wazee. Leo hii ninaomba nizungumzie ukatili na unyanyasaji unaofanyika kwa wafanyakazi wa ndani, wengi huwa hatulioni. Wafanyakazi wa ndani wanaendelea kunyanyaswa na kufanyiwa ukatili. Wafanyakazi wa ndani hawana likizo, wafanyakazi wa ndani hawaumwi, wafanyakzi wa ndani ndio madakatari, wafanyakazi wa ndani ndio ma– nurse, wafanyakazi wa ndani ndio kila kitu lakini bado wanalipwa mshahara mdogo. Nilikuwa naomba Wizara iwapitie na kuangalia jinsi gani wanaweza kulisaidia kundi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala pia la watumishi wa kada hii ya Wizara ya maendeleo ya jamii. Kada hii asilimia kubwa imesahaulika. Ukifika hata ndani ya halmashauri au kwenye ofisi yoyote, ofisi ambayo utaona haina gari itakuwa ni hiyo ya Maendeleo ya jamii, ofisi ambayo haina furniture nzuri ni hiyo ya maendeleo ya jamii, Ofisi ambayo watu wake wanachelewa kwenda kusomeshwa nje ya nchi ni hiyo ya maendeleo ya jamii. Ofisi ambayo yale mambo ya hovyo hovyo yanayotakiwa yawepo pale basi watapewa Wizara ya maendeleo ya jamii. Nilikuwa naomba Mheshimiwa waziri, alifuatilie suala hili na wale pia awatoe. Wale nao wapo kwenye ajira kama walivyo wengine. Wapewe mshahara mzuri, wapewe posjho nzuri na wao pia wasomeshwe ili waweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika hiyo hiyo maendeleo ya jamii, Vyuo vyao vingi vimechakaa na vilijengwa zamani. Sisi wakati ule ndio tulikuwa tunakwenda tunawafuata mama zetu tunaita wanaenda kwenye community center, huko ndiko walikuwa wanakwenda kujifunza vitu. Majengo yale tunaomba yakarabatiwe ili yawe ya kisasa yapendeze na watu wapate hamu ya kwenda kujifunza kutoka pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo nilikuwa naomba bajeti ya wizara hii iongezwe. Wizara hii ina mambo mengi kama unga wa ngano, kwenye chapati, kwenye mandazi, kwenye sambusa, kwenye nini, ndio wizara hii. Sasa iongezewe pesa ili iweze kufanya kazi zake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wizara hii pia ndio inayoongea na jamii yetu kwa haraka zaidi. Ninaomba wakaongee na wajasiriamali kuhusu suala la mikopo. Mheshimiwa Waziri, kama huna taarifa huko mitaani kuna mikopo inaitwa kichefu chefu, kuna mikopo inaitwa kibangala, kuna mikopo ya rusha roho, kuna mikopo ya komandoo, kuna mikopo ya miyeyusho, kuna mikopo pasua moyo. Haya yote ni mikopo ambayo wakinamama wanahangaika nayo na mingine inawadhalilisha. (Makofi)

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Nani amesimama? Mheshimiwa Felista Njau.

TAARIFA

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ninataka nimpe taarifa Mama anayechangia kwamba kuna mkopo unaitwa Kausha damu na sasa umesababisha wanawake wengi wameachika kwenye ndoa na kufirisika kabisa. Kwa sababu una riba kubwa na unalipa kila siku. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Angelina Malembeka, unapokea taarifa hiyo?

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, taarifa ya mikopo ya kausha damu ninaipokea. Ninaipokea kwa sababu hiyo ni moja ya ile mikopo ninayosema inawadhalilisha wakinamama. Kuna mikopo ambayo wakinamama unaenda kulipa mwili badala ya pesa. Kuna wanaume wamekaa huko standby wanaitwa mzee wa vikoba. Yaani mama akakope yeye kazi yake kulipa tu lakini analipa mwili, hii inatudhalilisha wanawake. Waziri, pita huko kwenye vikoba, pitia angalia wanakwendaje, tutakwisha magonjwa mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie pia suala la mabinti mama. Tunao mabinti wetu ambao wamepata watoto wakiwa na umri mdogo. Familia nyingi zimekuwa kwamba akishapata yule mtoto, wanamsusa au wanamtenga badala ya kumuweka karibu, kumwelekeza na kumsaidia. Jinsi wanavyozidi kumtenga ndivyo ambavyo wanatupa watoto, mara utasikia kaokotwa kwenye jalala, mwingine anampelekea bibi yeye mwenyewe aingie mtaani kwenye biashara nyingine.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tuwapunguzie mzigo wakina bibi kulea wajukuu. Basi wale mabinti-mama tukae nao tuongee nao, tuwape elimu ya ujasiriamali, tuwape mikopo wafanye kazi ili walee watoto wao waache kuwapeleka kwa bibi zao lakini pia nao waache kazi hiyo nyingine ya ziada wanayokwenda kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie pia maeneo ya vitambulisho vya wajasiriamali. Vitambulisho vilitolewa na baadae vikasitishwa wakasema wanaenda kuboresha, waziri atakapokuja naomba aje aniambie hivyo vitambulisho vimeboreshwa nini na vitapewa lini kwa hawa wajasiriamali? Kwa sababu huko mtaani usumbufu uko pale pale, haijulikani aliyepewa kitambulisho wala asiyepewa kitambulisho. Wanasumbuliwa maeneo ya biashara, wanasumbuliwa mara leseni, yaani ili mradi shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine kwa hao hao wajasiriamali na wafanyabiashara, ilizungumzwa kwamba watengewe maeneo kwa ajili ya kufanya biashara zao. Kuna halmashauri nyingine maeneo wametenga lakini wametenga tu eneo, vile vitu muhimu vya kupeleka pale havipo ni sawa sawa na hakuna. Unamwambia mtu kafanye biashara pale hakuna wateja, hakuna maji, hakuna usafiri, hakuna choo yaani ili mradi tu kero. Sasa, waziri atakapokuja hapa atwambie wapi ambapo wameandaa vizuri wakashinda? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuwapongeze wa Dodoma. Tumeona pale Dodoma aneo lao la wajasiriamali ni zuri na lina huduma nzuri. Sasa tunaomba na halmashauri nyingine zifuate hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo suala lingine la baba lishe na mama lishe. Hawa kila siku mimi nasema unaongea nao, kwa sababu nimekuona maeneo mengi ukiwa unafanya vikao na mama Lishe na baba Lishe na wajasiriamali wadogo wadogo kwenye vikundi. Pamoja na kuwatengea maeneo, je, yale maeneo mnayowatengea kweli yanawateja? Kwa sababu mtaji wao ni mdogo, unapompeleka kwenye eneo akafanye biashara wateja hana unajikuta kwanza hata kile chakula anakula mwenyewe na watoto wake. Kwa hiyo, hafanyi biashara. kwa hiyo, mnapowapangia maeneo ya kufanya biashara muangalie je, hapa wateja wapo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mchango wangu huu wa leo ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia kidogo katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Masauni na Naibu wake Mheshimiwa Sagini na timu yao yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuilinda nchi yetu na kulinda mali za wananchi na kwa kuonyesha msimamo wa kutetea wananchi wake hususani nikitolea mfano kwa jinsi alivyochukua hatua za haraka kwenda kupeleka usafiri Sudani Kusini na kuwachukua wanafunzi wa Tanzania ambao walikuwa kule na kuwarudisha nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe pongezi pia kwa Trafiki wa Zanzibar, Trafiki wa Zanzibar wamekuwa trafiki marafiki, Trafiki wa Zanzibar unaweza ukamfuata hata kama umepotea njia akakuelekeza, nenda njia fulani. Trafiki wa Zanzibar anaweza akakusimamisha, akakwambia usipite njia hii ina foleni pita njia hii. Trafiki wa Zanzibar anaweza akasimama kwenye zebra akasimamisha magari akatoka mwenyewe kwenda kushika wanafunzi au watoto kuwavusha mpaka upande wa pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo mengine tumeona trafiki yuko kwenye zebra lakini haangalii kusimamisha magari ili watu wapite macho yake yako kulia anaangalia daladala linalokuja litafanya nini ili nipige mkono. Kwa hiyo hilo pia Mheshimiwa Waziri aliangalie, kuna baadhi ya matrafiki hawako sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia Trafiki wa Chanika, Chanika kuna kiongozi anakaa kule, si vizuri kumtaja kwa nafasi lakini huwa anakwenda, lakini kituo kile hakina raider ya kuongoza misafara, unakuta kwamba wanatumia tu mikono na taa na wakati kiongozi mkubwa sana huwa anaenda kule. Sasa naomba Wizara hii iangalie kupeleka raider kwa Polisi wa Chanika, barabara ile ni kubwa, ina maroli mengi ina mabasi mengi, sasa ni vizuri tuangalie usalama zaidi wa viongozi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitoe pongezi kwa Jeshi la Magereza kwa sasa hivi wanatumia vizuri nafasi za wafungwa. Zamani tulikuwa na kazi tu ya kuwalisha na kuwavalisha nguo kazi hazionekani, lakini sasa hivi tumeona kwamba maofisi mengi na vituo vingi vya Magereza majengo yanajengwa kuna ma-hall kuna nini, magereza wanafanya kazi unajua kweli huyu sasa akitoka hapa akashajifunza kitu anaenda kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaniona mtu wa pongezi sana, natoa pongezi sana kwa sababu haya yanayofanyika yanaonekana, nipongeze Jeshi la Uhamiaji katika utaratibu mzima wa utoaji Passport kwa sasa hivi kwa maana hati za kusafiria. Zamani ukitafuta hati ya kusafiria yaani unahangaika kama unatafuta kumtoa mtu figo ukaweke kwako, sasa hivi Passport ukisema dakika mbili unaambiwa baada ya muda fulani njoo uchukue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeliona hilo Dodoma, tumeliona hilo Dar es Salaam japo kuna maeneo mengine yana matatizo kidogo, basi niombe wawasaidie hususani katika masuala ya kompyuta ikitolewa mfano katika Mkoa wa Iringa, kompyuta zao ni za kizamani, wawarekebishie wawape za kisasa na maeneo mengine ambayo bado yana kompyuta za kizamani, ili waweze kufanya kazi zao vizuri, watu wapate Passport mapema. Nasema hivi kwa sababu kuna wakati mwingine Passport unapata kidharura dharura, siyo kwamba kila anayechukua Passport kwa ajili ya sterehe zake. Kwa hiyo niwapongeze kwamba wameboresha kwa sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe pongezi vile vile kwa Trafiki wa Makumbusho Dar es Salaam, yule kijana anajituma, ile kazi inaonekana kaipenda na ameingia pale kwa dhati, anaongoza magari kwa mbwembwe, watu wanapita pale wanamtunza, lakini nafikiri kuna wengine wameenda kwenye upolisi hawana jinsi ili mradi tu niende nizibe pengo. Kwa hiyo napenda hao mapolisi kweli wanaoenda huko waangalie, huo upolisi wanautaka au wamekwenda tu kwa sababu hamna kitu kingine cha kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa polisi wetu pamoja na pongezi zote tunazowapa, kuna maeneo ambayo wanatupa kero, unaanza na king’amuzi, basi akimshika mmoja mwenye tisini yatapita magari hata ishirini yote yanaonyesha king’amuzi tisini tu, tisini hiyo hiyo haibadiliki wanaoneshwa hiyohiyo. Kama hivyo ving’amuzi vibovu vikatengenezwe au vinunuliwe vipya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, wana mchezo wa kujificha hawa, utaona tu ghafla kakurupuka kwenye mihogo, sasa wewe Bwana Shamba? Uko kwenye mihogo ulifuata nini? Kaa barabarani tukuone kama kuna tatizo tusimame tukwambie, bwana tusaidie hapa, kuna mwingine anamtaka trafiki amuulize hivi kutoka Gairo mpaka manyoni ni kilomita ngapi, lakini yeye yuko kwenye mihogo ghafla tu anaingia ili mradi tu uvunje sheria. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, trafiki wana ucheleweshaji usiokuwa na sababu, wanaweza wakasimamisha mabasi ya abiria, malori na kadhalika, halafu mwenyewe anakaa anachati pale anasubiri dereva au konda atoke amfuate pale akamuulize. Sasa wanawatia hasira madereva, wakitoka pale wanatoka spidi, matokeo yake tunasababisha ajali mbele. Ni afadhali anaposimama aongee naye palepale wamalizane palepale kama kuendelea na safari aendelee kama ni kumwandikia amwandikie badala ya kumsimamisha kwa muda mrefu na kumpotezea muda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna matrafiki wengine ni walevi, asubuhi tu analewa. Mimi nimekutana naye Morogoro, kanisimamisha nimesimama, kaniuliza hii namba ya wapi nikamwambia hii namba ya usajili wa Zanzibar, akauliza nitajuaje kama Zanzibar? Dereva wangu akamjibu akamwambia si umeona bendera hiyo ya Mbunge? Akasema, aah, bendera hata mimi ninayo kiunoni, lakini kutokana na harufu yake nilivyomskia nikajua mlevi nikamwambia achana naye tuondoke. Sasa walevi kama wale Wizara iwaangalie asubuhi asubuhi isiwe inawapangia kazi huko barabarani, wanatuletea vituko. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kuna kazi nyingine ambazo zinakuwa kioo cha jamii wakiwemo Mapolisi, Wanajeshi kwa ujumla kuna Walimu, kuna Madaktari hata Wabunge yaani ni kazi ambazo zinaenda watu wanakuangalia kioo cha jamii. Sasa tunaposikia Polisi yuko katika ule mchezo kwa kweli wanatutia mashaka. Unasikia mtoto kalawitiwa au kabakwa, unamchukua unataka umpeleke polisi, halafu unakuja unasikia polisi mwenyewe ndio walewale, wanatukatisha tamaa na watatugombanisha kwa sababu ukishamchukua mtoto aliyelawitiwa ukampeleka polisi, kumbe polisi mwenyewe ndio yuleyule anakuona mbaya wale waliompeleka huyo mtu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba maadili kwenye Jeshi la Polisi na wengineo liangaliwe kwa kina, kwa sababu licha ya kutia aibu, lakini wanatukatisha tamaa, halafu baadae wanatuambia mbona mnamalizana wenyewe kijamii jamii hukohuko nyumbani, sasa huko polisi tukienda na mambo yenyewe ndio hayo inakuwaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote niseme kabisa pongezi nyingine kwa Waziri na Mheshimiwa Rais, nyumba za askari sasa hivi nyingi zimeboreshwa tofauti na zamani. Zamani mpaka tunajiuliza yaani chumba kimoja wanapishana kwa mapazia unajiuliza wanapataje watoto pale, lakini sasa hivi tunashukuru nyumba za maaskari zimekuwa nzuri, zinaheshimika, wamewapa staha. Naomba Wizara waongeze nguvu yale maeneo mengine ambayo hayajapata nyumba, basi wajengewe waendelee kuwa na staha. Pamoja na hayo bado napendekeza vifaa zaidi vinunuliwe vya kisasa kwa ajili ya askari wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa fursa na mimi kuchangia katika Wizara hizi. Pia, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwenye wingi wa rehema kwa kuniwezesha kuweza kuongea katika siku hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya hapa nchini na sisi wote tunamuunga mkono tunasema mitano tena. Niwapongeze Mawaziri wa Wizara zote mbili, Naibu Mawiziri wao, Makatibu Wakuu na watendaji kwa ujumla kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa Vazi la Taifa. Vazi la Taifa limekuwa ni mjadala na swali ambalo tumelizungumza kwa kipindi kirefu tangu Bunge la Kumi na Moja tumezungumza na hili Bunge la Kumi na Mbili, nina wasiwasi tunaweza tukafika wengine mpaka Bunge la Kumi na Tatu Vazi la Taifa halijapatikana lakini ni pesa nyingi zimetumika, vikao vingi vimefanyika, posho nyingi wamelipana kwa ajili ya kutafuta Vazi la Taifa kana kwamba mpaka sasa hivi Watanzania hatujui kuvaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafikiri Vazi la Taifa kinachotakiwa ipatikane nguo ya stara yenye ustaarabu, yenye heshima na inayoonyesha unadhifu ambayo inaweza ikavaliwa na rika lolote kwa umbo lolote na nguo ambayo inaweza iikatengenezwa na kwa malighafi yoyote ina maana kwa cotton kama tetroni kama ni ginger, kwa kitenge itapatikana na hiyo nguo iweze kuvaliwa mahali popote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafikiria kwa mavazi anayovaa Mama yetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan inatosha kabisa kuwa vazi la Taifa, kwa sababu zile nguo zina stara, zina ustaarabu, zina heshima na unadhifu wa hali ya juu. Vazi la kanzu na ndani suruali hata mwanaume ameweza kuvaa tukawa tunashindana tu huku juu mbwembwe huyu akaweka vifungo, huyu akaweka zipu lakini nguo ya Taifa ikapatikana. Haiwezekani miaka kumi tunatafuta Vazi la Taifa. Naomba pafanyiwe kazi tujue nguo gani tunavaa mpaka sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nilizungumzie ni juu ya mdundo wa Taifa. Tanzania hii tuna makabila zaidi ya 120 lakini nilivyouliza mdundo wa Taifa nikaambiwa mtaalamu amepatikana anataka kuchanganya midundo ya makabila yote ili upatikane mdundo, hiko kitu hakiwezani. Kuna Mikoa ya Kaskazini ngoma zao zinachezwa kuanzia mabega kwenda juu. Kuna wale wa Kusini ngoma zao zinachezwa kuanzia kwenye kiuno kwenda chini wewe unataka kuniambia ngoma ya Mngoni utaenda kumchezesha Mmasai, unataka kuniambia ngoma ya Mmakonde utaenda kumchezesha Mpare, unataka kuniambia ngoma ya Muhaya unaweza kumchezesha Mpemba? Kwa kweli hicho kitu hakiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo midundo ya Taifa ambayo ipo automatically imefika ipo. Nikitolea mfano ule mziki unaopigwa kabla ya taarifa ya habari ya Zanzibar popote ukipigwa ule wanajua sasa taarifa ya habari huo unafaa kuwa Mdundo wa Taifa. Kuna mziki unaopigwa na Redio Tanzania wa Mourice Nyunyusa ule ngoma 12 zile ukipigwa kokote tunajua hii ni taarifa ya habari inakuja. Kwa nini hiyo midundo hiyo isitafutwe ikasemwa hii ni Midundo ya Taifa badala ya kwenda kutafuta makabila 120 utuchanganyie utuambie mziki, huo mziki gani tunaenda kudundia wapi, tutachezaje kwanza? Mimi ninaomba hiyo Kamati iliyotengenezwa kwa ajili ya Mdundo wa Taifa japo imesema imemaliza kazi yake bado kuzindua mimi naona tuangalie huo mdundo tunaotengeneza una asili gani, hizo mbili tu nilizotaja mtu anajua ngoma hii asili yake mahali fulani na ilipigwa na fulani na ina historia yake badala ya kutuchanganyia vyombo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la Mfuko wa Wasanii; Kwanza kwenye upande wa sanaa nimeona hata huo mfuko umeangalia zaidi kwa waimbaji siyo kwamba sitaki wapewe, kwa waimbaji, lakini tumesahau kuna waumbaji, wafinyanzi, watengeneza mikeka kama jamvi, vikapu, matenga, wasusi na wasokotaji kamba, wapaka rangi, wachoraji na wabunifu yani designers hao naona amesahauliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kusahauliwa kwao sasa hivi wazungu wanakuja, wanajifunza huko kusuka mikeka, kutengeneza makapu, kutengeneza sijui matenga halafu sisi tunaletewa ya plastiki vikapu vya plastiki, matenga manini tunapeleka mpaka kijijini. Ule utaalamu kule unakufa, hakuna watu wa kuwafundisha na wale ambao wapo hatuwawezeshi, matokeo yake baada ya miaka kadhaa watauambia hizo plastic zinaleta kansa na zinachafua mazingira, makapu ya kwetu watatuletea watatuuzia tena wakati wale wenye uwezo wa kutengeneza wameshapotea na hiyo fani haipo. Mimi napendekeza Serikali iwaone hawa wenye ufundi wa jadi wawasaidie ili ile fani iendelee na tuepukane na haya mambo mengine ya kuletewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika lugha yetu ya Kiswahili, sasa hivi Kiswahili kimekua na kimekua sana na kimekua kwa kasi. Nipongeze BAKITA kwa kuleta kamusi mpya kubwa na yakisasa ambayo imechanganua vitu vingi sana. Kuna wakati BAKITA walikuwa wanatoa baadhi ya maneno ya Kiswahili alafu wanatoa tafsiri yake kwamba neno hili maana yake hii tunaona kwenye mtandao sioni sijui kwanini wameacha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu na hofu yangu ni kwamba hiki Kiswahili kinachokua kuna maneno ya Kiswahili ambayo yana maana tofauti wao wanayatengeneza wanavyotaka wenyewe halafu mtu unashindwa hata kutamka mbele za watu lile neno wakati unajua ni neno la kawaida la Kiswahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani mtu anaweza akakwambia mimi napenda msondo, napenda sikinde, napenda taarabu; lakini siku hizi ukisema mbele za watu napenda taarabu wanakushangaa kutokana na tafsiri waliyoiweka huko mtaani. Sasa BAKITA iwe inatoa amelezo kamili kwamba lugha hii maana yake hii na lugha hii maana yake hii nah ii siyo sahihi wanavyonyamaza kimya lile neno linakua na watu wanaona la kawaida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije nizungumzie kwenye suala la michezo ya kubahatisha. Nakumbuka mwaka 2021 tulikaa hapa kufanya marekebisho ya Sheria katika Baraza la Michezo ambapo tulikubaliana 5% ya mapato yanayopatikana kwenye hii michezo ya kubahatisha ipelekwe kwenye Wizara hususani kwenye Baraza la Michezo la Taifa ili kufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninahisi mpaka sasa hivi hizo hela haziendi na kama zinaenda zinaenda kidodo sasa basi Serikali ituambie kwanini hizo pesa haziendi wakati Sheria imeshapitishwa, Wizara kwa nini inashindwa kupokea hiyo pesa wapelekewe hizo pesa waweze kufanya kazi badala ya kuwa kila siku tunawalaumu tu kwenye michezo kumefanya hivi kumefanya hivi wakati pesa hatupeleki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shida hiyo niwapongeze watu wa Wizara kwa kweli kwa mwaka huu wamejitahidi timu zetu nyingi zimefuzu japo huko mbele ya safari tumekosa bahati. AFCON wanaume wameenda Ivory Coast walifuzu japo kule tulipoteza lakini kuna AFCON wanawake wanaenda Morocco kuna…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana muda wako umeisha malizia.

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba dakika mbili za kumalizia. Kwa ufupi nizipongeze timu zote lakini mwisho kabisa nimpongeze Mama Samia Suluhu Hassan kwa hoja ya Kigoma Mjini kwa yule mtoto Ally Haji ambapo pamoja na matatizo yalivyojitokeza Mama Samia Suluhu Hassan Mheshimiwa Rais wetu aliyeamua kuonyesha Umama wake, ameamua kumtibia yule mama kujenga nyumba kwa yule mama kumpa mtaji wa biashara na kumsomesha, lile jambo ni zuri tunampongeza tunamuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba Wizara ya Maendeleo ya Jamii kwamba tunapowakuta watoto mitaani tupate fursa ya kukaa nao, tuwahoji, tujue wana matatizo gani ili tuweze kuwasaidia. Ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha na mimi kuwepo hapa, pili nichukue nafasi hii kuwapa pongezi Wabunge wenzetu wa UKAWA kwa kurudi Bungeni. Nilikuwa najiuliza wenzetu hawa walitoka kwa hiari yao na wamerudi kwa hiari yao haya wanayoyasema wangeyasemea wapi kama wangekuwa nje. Kwa hiyo, kwa kurudi kwao nimefurahi sana kwa sababu hata sisi michango yao pia tunaipenda yapo mambo tunajifunza kutoka kwao. Kwa hiyo, nilikuwa najiuliza wanapokaa nje hayo maneno watasemea wapi?(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuendelea pamoja na pongezi zao wanazozikataa nimpongeze kipekee Mheshimiwa Magdalena Sakaya kwa kutoa taarifa kwa sababu mara zote michango yake pia huwa mizuri ambayo pia inaisaidia Serikali. Sasa tulikuwa tunajiuliza kama na yeye anatoka inakuwaje sasa humu ndani, sisi tunapenda michango yote ya pande zote mbili ili Serikali iweze kuifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi niwapongeze Wabunge wenzangu wa Chama cha Mapinduzi ambao hawajawahi kununa wala kutoka ndani ya Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango wangu wa Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wenzangu wamechangia mengi, lakini na mimi ninayo machache ya kuongezea nyama na pale Serikali ambapo itaona inafaa basi nao watayafanyia kazi. Kabla ya kutoa mchango huo wapo Wajumbe kadhaa ambao wameizungumzia suala la ubaguzi humu ndani, lakini wao wenyewe ndiyo wamekuwa wabaguzi wa kwanza kwa kuhoji kwa nini Wabunge wa Zanzibar wanachangia hoja hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wanaotoka Zanzibar ni Wabunge halali wa Bunge la Muungano wa Tanzania sawa sawa na aliyetoka Rombo, Mwanza, Singida, au Kagera, kwa sababu wote wana majimbo yao na waliokuja kwa mikoa yao wamekuja kwa Mikoa yao ambayo iko ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wanapohoji kwa nini Wabunge wa Zanzibar wanajadili hili wanajisahau wao kwa nini wali-panic Jecha alipofanya vitu vyake kule. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala haya ya kujifanya huelewi tofauti ya Baraza la Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Muungano ndiyo walioyafanya waponze wenzao mpaka wakakosa Madiwani na Wawakilishi Zanzibar yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusiana na suala la hii sheria ambayo wanahoji kwa nini itumike Bara pake yake isitumike Zanzibar. Mimi ninaamini hii siyo sheria ya kwanza ziko sheria nyingi ambazo zimetungwa zinatumika Bara peke yake na Zanzibar hazitumiki. Nikitolea mfano kuhusu umilikaji wa silaha za moto, Zanzibar raia yeyote haruhusiwi kumiliki silaha yeyote lakini Bara wanaruhusiwa, ni Bunge hili lilipitisha hawa hawakuliona au wanakuja kushangaa hii tu ya habari? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado niongelee kuhusiana na suala la adhabu, kwa upande wangu nimeona adhabu hii ni kubwa, kwa sababu hawa wanahabari wetu katika kuleta habari zao tunaweza tukajistukia magereza zote zimejaa wao, kule hatutaweza kuwalisha, hatutaweza kuwatunza, ni afadhali basi adhabu hii ipunguzwe, isipokuwa iongezwe kwa yule mtu wa kwanza mtoa habari, kwa sababu yule mtoa habari wa kwanza kama ataachiwa itakuwa anaendelea kutoa habari na wenzake wanaendelea kuzipotosha, sasa ni vizuri yule wa kwanza kabisa ndiyo apewe adhabu kubwa zaidi kuliko wale wengine wanaozambaza zile habari hata kama ni za upotofu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuchangia hayo naona Muswada huu upo vizuri kwa sababu umetoa haki ya kupata taarifa kama Katiba ya nchi inavyotaka. Sasa hivi hali ilivyo unaweza kwenda kuomba taarifa na usipewe na huna wa kumuuliza na unaweza usijibiwe na yakaisha kimya kimya. Lakini kwa Muswada huu ambao tunapitisha bado itampa nafasi kubwa mwananchi kupata taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muda ni mfupi umesema tutumie dakika 10 nina wenzangu ambao wana michango mizuri zaidi ninashukuru kwa kunipa nafasi.