Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Ritta Enespher Kabati (136 total)

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.
Kwa kuwa Wilaya ya Kilolo ilipata kuwa hadhi ya Wilaya toka mwaka 2002 lakini majengo mengi katika Wilaya bado hayajakamilika, kama Hospitali ya Wilaya bado wanatumia Hopitali ya Mission, Makao Makuu ya Polisi bado hayajajengwa kwenye Wilaya yake na vilevile Mahakama bado hakuna…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa naomba uulize swali!
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, je, huwa vigezo gani vinatumika katika kuweka mipango kujenga hizi Wilaya? Kwa sababu Wilaya za zamani bado hazijatimiziwa majengo yote na zinaanzishwa Wilaya mpya, nilitaka nijue vigezo gani vinatumika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba miundombinu ya Wilaya ya Kilolo bado haijakamilika, siyo Wilaya ya Kilolo peke yake isipokuwa ni Wilaya mbalimbali, vipaumbele vinavyotumika kwanza mazoezi yote yanaanza katika mchakato wa bajeti, na ndiyo maana mwaka huu ukiangalia tuna karibu Wilaya zipatazo 44, hizi ni Halmashauri na Wilaya mpya mbalimbali ambazo tumezipa fedha.
Hali kadhalika tunaangalia upungufu katika maeneo mbalimbali. Imani yangu kubwa ni kwamba suala la Kilolo limesikika na kwa sababu tuna Wilaya mpya na Halmashauri nyingine tunaendelea katika ujenzi wa miundombinu, tukifika katika mafungu yetu ya Mikoa utakuja kubainisha kwamba jinsi gani kila Mkoa katika mafungu yake yameweza kuelekezwa. Ile sehemu ambapo miundombinu haijakamilika lakini Wilaya ambazo ni mpya tunaanza kuziasisi tena upya, jinsi gani tume-allocate funds katika mwaka huu wa fedha ili tuweke hali halisi ya kuhakikisha kwamba wafanyakazi katika maeneo hayo waweze kufanyakazi katika mazingira rafiki.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA(MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE): Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana yaliyotolewa na Naibu Waziri Jafo, nilitaka tuelewane kwenye jambo hili la uanzishaji wa maeneo mapya ya utawala.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni gumu na sote hapa tunafahamu kwamba maombi haya ya kuanzisha haya maeneo yanatokana na mahitaji ya wananchi. Lakini ni sisi wenyewe kwenye maeneo yetu ndiyo huwa tunaanzisha haya. Kwa kuwa maombi haya yanakuja mengi na wakati mwingine Serikali siyo rahisi sana kupata fedha kwa mara moja kujenga mahitaji yote ya Makao Makuu ya Halmashauri au Wilaya ni lazima tuvumiliane. Ni lazima tuvumiliane twende kidogo kidogo na ndiyo maana Serikali imekuwa ikitenga milioni 500, tunaamini tukifanya hivyo kwa miaka mitano, miaka minne, tunaweza tukakamilisha majengo yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuvumiliane kwa sababu Wabunge wengi wanakuja kuniona wakiwa na maombi mapya ya maeneo mengine ya utawala, sasa tukianza kuulizwa maswali kama kwa nini tunakuwa hatujajipanga na tunayaanzisha, kuna wengine hapa mmeahidi huko mlikotoka kwamba sisi tutahakikisha hapa panakuwa Mji Mdogo, sisi tutahakikisha tunakuwa na Halmashauri, sisi tutahakikisha tunakuwa na Wilaya.
Sasa tuvumiliane na tuende pamoja na tuamini kwamba kadri Serikali itakapopata uwezo tutakuwa tunafanya, lakini jambo hili ni gumu.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Kwa kuwa wanawake wengi sana wanaoishi vijijini hasa katika Mkoa wetu wa Iringa, wamekuwa wakipata shida sana wanapotafuta msaada wa kisheria; na kwa kuwa mashirika haya mengi yako mijini.
Je, Serikali inawasaidiaje wananchi ambao wanakaa mbali na miji ili angalau hata kupeleka mobile elimu ili waweze kufikiwa?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wanawake wengi walioko vijijini wanakabiliwa na changamoto ya kupata msaada wa Sheria, lakini nataka nimthibitishie kwamba kwa sasa hivi Waziri wa Katiba na Sheria tayari ameshaleta mapendekezo ya Kutunga Sheria ya Msaada wa Kisheria ambapo itahakikisha msaada wa kisheria unapatikana kwa wananchi wote wenye mkahitaji, wakiwemo wanawake walio vijijini. Kwa hiyo, ni suala ambalo tayari Serikali ya Awamu ya Tano inalifanyia kazi na tunataka kumuahidi kwamba ndani ya siku chache tutakuwa na sheria, hivyo wanawake wataweza kupata.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili; tayari tunazo NGOs mbalimbali ambazo zinafanya kazi ya kutoa Msaada wa Sheria kwa wanawake, ikiwemo Chama cha Wanasheria Wanawake na Chama cha Wanawake Wanahabari. Kwa hiyo, tunazo taasisi mbalimbali ambazo zinatoa msaada wa sheria kwa wanawake.
RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba kuuliza maswali madogo mawili.
Kwa kuwa Wilaya ya Kilolo imezungukwa na mito ya Ruaha, Mto Rukosi; ni kwa nini Serikali isivute maji kutoka katika mito hiyo kuliko kuchimba visima ambavyo vimekuwa vikichimbwa, lakini havitoi maji?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa visima…
SPIKA: Hilo, swali la kwanza ulilouliza ni kwa niaba ya kaka au? (Kicheko)
Mheshimiwa endelea!
MHE. RITTA E. KABATI: Swali la pili, kwa kuwa visima virefu huwa havina uhakika sana wa kutoa maji na mara nyingi vimekuwa vikiharibika! Ni kwa nini Serikali isielekeze nguvu kwenye kuchimba mabwawa badala ya kutumia fedha nyingi sana katika kuchimba hivi visima ambavyo mara nyingi vimekuwa havina uhakika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKAL ZA MITAA): Mheshimiwa Spika, swali la kwanza lilikuwa ni kwa nini sasa tusitumie fursa za mito ambayo inapita katika Jimbo la Kilolo badala ya kwenda kuchimba visima virefu. Katika utekelezaji wa miradi ya maji, kwanza wataalam wanaangalia au wanafanya analysis, ni chanzo gani cha maji ambacho kitaweza kusaidia, lakini utafiti huo vilevile unaendana na bajeti.
Mheshimiwa Spika, kuna maeneo mbalimbali ambayo yamebainika kwamba kumeenda kuchimbwa visima virefu, lakini sehemu zingine kuna fursa za maji. Hili naomba nikiri hapa wazi kwamba, watu wengi mbalimbali hasa wa kutoka maeneo mbalimbali ambayo kuna mito mirefu au maziwa, kama watu wa Kanda ya Ziwa wanasema kwa nini tuchimbiwe visima badala ya kutumia vyanzo vilivyopo. Naamini katika Programu ya Maji ya Awamu ya Pili ambayo sasa inaanza, Watalaam wetu, wataangalia katika sehemu ambayo kuna fursa ya vyanzo vikubwa vya maji hasa mito viweze kutumika vizuri kutokana na bajeti iliyopo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimthibitishie Mbunge kwamba katika Awamu ya Pili ya Mradi wa Maji, watalaam wetu wataenda mbali zaidi kuangalia fursa. Ndiyo maana tulisema pale awali kwamba maeneo yote yanayozungukwa na vyanzo vikubwa vya maji, basi watalaam itabidi wajielekeze huko kuona jinsi gani ya kufanya ilimradi kupata maji ya uhakika na kuhakikisha fedha inatumika vizuri.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni kwa nini sasa kuchimba visima virefu badala ya kuchimba mabwawa. Mara nyingi sana watalaam wanazungumza kwamba maji ya kisima kirefu, kitaaluma au kitalaam, ukiyatoa yanakuwa maji safi na bora, kwa sababu yanakuwa hayana contamination, lakini maji ya bwawa maana yake yanataka ufanye treatment.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, imeonekana wazi, sehemu zingine visima virefu kweli vimechimbwa, lakini hatukupata maji. Kwa sababu uhitaji wa maji ni mkubwa na sehemu zingine water table inasumbua sana, naamini sasa, ndiyo maana katika mkutano wetu wa pili tuliofanya tathmini pale Dar es Salaam, tulielekeza kila Halmashauri, ikiwezekana kila mwaka twende katika uelekeo wa mabwawa kwa sababu maeneo mengi mbalimbali tuliyochimba visima virefu ni kweli wakati mwingine tulikosa maji na wakati mwingine miradi hii inaharibika. Vitu hivi vyote vitakwenda sambamba kwa pamoja kuangalia engineering specifications ya maji inasemaje kwa ajili ya kuelekeza wananchi wapate maji bora na salama.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize Sali dogo tu la nyongeza. Kwa kuwa njia mojawapo ya kupunguza hivi vifo vya mama na mtoto ni pamoja na kuboresha mfumo wa referral, yaani kutoka kwenye Vituo vya Afya, ama kwenye Hospitali za Wilaya kwenda kwenye Hospitali ya Mkoa; na kwa kuwa vituo vyetu vingi sana katika Mkoa wetu wa Iringa havina magari ya kubebea wagonjwa na vipo katika miundombinu mibaya sana ya barabara: Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kila Kituo cha Afya kinapatiwa gari ili kupunguza hivi vifo vya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba taarifa hizi zimfikie Mheshimiwa Ritta Kabati na Wabunge wote ambao wangependa kupata magari ya ambulance kwenye Halmashauri zao, kwamba kwanza jukumu la kununua magari haya lipo kwenye Halmashauri zenyewe. Waheshimiwa Wabunge kwa kuwa ni sehemu ya Halmashauri hizi, kwenye mipango yao ya bajeti tayari tutakapomaliza Bunge hili utaratibu wa mchakato mzima wa bajeti utaanza, basi Wabunge wahudhurie vikao hivyo na waweke ambulance kama kipaumbele cha kwanza kwenye bajeti zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hivyo, sisi Wizara ya Afya, tutaendelea kuwaomba na kuwashirikisha wadau wa maendeleo watupe ufadhili. Kama tutafanikiwa kupata ambulance, basi tutazigawa kwenye hospitali zetu nchini.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Sera ya Serikali ni kuunganisha barabara za mikoa na za wilaya kwa lami lakini katika Mkoa wetu wa Iringa, Wilaya ya Kilolo ni wilaya ambayo toka mwaka 2002 imepata hadhi ya kuwa wilaya mpaka leo hii haijaweza kuunganishwa kwa lami kutoka yalipo makao makuu. Ni lini sasa Serikali itaunganisha wilaya hii na makao makuu kwa lami ili hii sera iweze kutimia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Wilaya ya Kilolo haijaunganishwa na barabara ya lami kama ambavyo Mbunge wa Kilolo na Mbunge wa Viti Maalum Mheshimiwa Ritta Kabati wamekuwa wakifuatilia suala hili ofisini kwetu na nyakati zote tumekuwa tukiwaahidi kwamba tutafuatilia. Kwanza Mheshimiwa Rais alipopita lile eneo hiyo pia ilikuwa ni sehemu ya ahadi yake licha ya kwamba hii ni ahadi ya kiujumla kwa wilaya zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie maadam dhamira yetu ni kuhakikisha miundombinu inajengwa na ahadi zote za viongozi wetu tunazitekeleza atupe muda ili tutakapopata ratiba kamili ya suala hili tutatekeleza. Mnafahamu tumeanza kwa kiwango fulani, ni kiwango ambacho hakitoshelezi nakubali kama ambavyo Mheshimiwa Mwamoto amekuwa akinisukuma kila wakati kuhusu hilo suala. Niwahakikishie wote Mheshimiwa Mwamoto na Mheshimiwa Ritta Kabati kwamba ahadi hiyo tutaitekeleza kama ambavyo tumeongea nao tukiwa maofisini.
MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kuuliza swali fupi tu. Kwanza niipongeze Serikali kwa kuanzisha Kitengo cha Matibabu ya Figo katika Hospitali ya Benjamin Mkapa hapa Dodoma. Hata hivyo, nimeona Hospitali ya Muhimbili pia ina kitengo kinashughulikia matibabu ya figo. Ni kwa nini Serikali isiweke eneo moja, kwa mfano hapa Dodoma washughulikie tu mambo ya figo na kule Muhimbili washughulikie tu mambo ya moyo? Pia nimeona tengeo katika bajeti, sasa hapa ni kama kuharibu rasilimali, naomba jibu.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ni kwamba, tayari Serikali ndicho inachokifanya, hospitali ya kisasa kabisa ya Benjamin Mkapa Ultra-Modern Hospital itabobea zaidi kwenye kutoa tiba mahsusi ya magonjwa ya figo. Tutaanzia kwenye hizi tiba ambazo sasa hivi tunazo kwenye hospitali nyingine za dialysis kwa maana ya kusafisha figo na tunakwenda mbele zaidi hadi kuanza kufanya huduma za kupandikiza figo (transplant) na hayo yatafanyika kwenye Hospitali ya Benjamin Mkapa hapa Dodoma.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nina maswali tu madogo mawili ya nyongeza.
Pamoja na askari wa Iringa kuishi kwenye mazingira magumu sana, lakini zaidi ya nusu ya askari wanaishi nje ya makambi yao yaani uraiani. Pia katika Mkoa huo wa Iringa, Wilaya ya Kilolo Serikali haijaweza hata kujenga jengo lolote la ofisi wala makazi ya askari na katika majibu yake Serikali imesema kwamba itakuwa inajenga kadri itakavyokuwa inapata fedha.
Je, Serikali ipo tayari sasa kutoa kipaumbele kwa Mkoa wetu wa Iringa ili askari wetu waweze kuishi kwenye mazingira bora yajengwe mapema sana? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa askari wa Mkoa wa Iringa wanadai posho na stahiki zao kiasi kikubwa sana cha pesa na Serikali imesema kwamba bado wanafanya uhakiki. Je, ni lini sasa uhakiki utakamilika ili askari wetu wa Mkoa wa Iringa waweze kupata stahiki zao na posho kwa sababu familia zoa zimekuwa zikiishi kwa shida sana na hasa watoto na wake za askari? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, wakati tunakamilisha mchakato wa ujenzi wa nyumba za askari ule ambao nimekuwa nikiuzungumza hapa Bungeni kila siku ambao pia utahusisha na Mkoa wa Iringa tunajipanga kutumia rasilimali za ndani pamoja na rasilimali zilizopo katika maeneo husika pamoja na rasilimali watu ili kupunguza tatizo au changamoto za makazi kwa askari wetu na vituo vya polisi.
Mheshimiwa Spika, nataka nichukue fursa hii kwanza kabisa na kwa dhati nimpongeze Mheshimiwa Ritta Kabati kwa jitihada zake kubwa sana ikiwemo ujenzi wa Kituo cha Polisi Iringa, ambapo sasa hivi nguvu zake anazielekeza maeneo ya Kilolo, lakini kwa kutambua kwamba Mheshimiwa Mbunge amefanya kazi kubwa sana pale Iringa ya ujenzi wa kituo nataka nimhakikishie kwamba tutakuwa pamoja na yeye tutashirikiana naye ili tuweze kuona kwa haraka sana tutatumia mpango huu wa matumizi ya rasilimali katika eneo husika ili kupunguza changamoto ya makazi pamoja na vituo vya polisi.
Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya kikao hiki cha Bunge tukae kwa pamoja tushauriane tuone iko vipi kwa haraka sana mpango huu ambao tumeubuni hivi karibuni tunaanza kutekekeleza kwa Kilolo.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusiana na lini ukaguzi utamalizika. Naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba tunakamilisha ukaguzi haraka iwezekanavyo ili malipo haya yaweze kulipwa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu na nimpongeze sana niongezee tu kwa kumpa assurance Mheshimiwa Mbunge ambaye jambo hili amekuwa akilifuatilia kwa umakini sana la maisha ya polisi na vitendea kazi vyao kwamba tarehe 9 Septemba, 2016 wale wenzetu ambao tulikuwa tunaongea nao kuhusu mkataba wa ujenzi wa nyumba za askari kiongozi wao mkubwa atakuja na atakutana na IGP pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara na baada ya hapo tutabakiza mawasiliano ya ndani ya Serikali kwa ajili ya kwenda kwenye utekelezaji wa jambo hilo.
Mheshimiwa Spika, la pili Wizara tumeamua kwenda na jambo hili sambamba kwamba jitihada zitakazofanyika za kibajeti tuzioanishe na jitihada za rasilimali tulizonazo ndani ya taasisi zetu hizi na nimeelekeza mikoa yote wafanye tathmini ya kila mkoa tuna wafungwa wangapi wanaoweza kufanya kazi za kufyatua tofali na wafanye tathmini ya vitendea kazi vinavyoweza kutumika kufyatulia tofali hizo na aina ya tofali ambazo zinatakiwa, lakini pia na kutumia bajeti kidogo zilizopo kwa ajili ya vitendea kazi vingine ambavyo vitatakiwa kama cement ama nondo kwa ajili ya kuanza miradi hiyo katika maeneo ambayo kazi hiyo si kubwa sana kwa ajili ya kupunguza tatizo hili sambamba na jitihada za kibajeti ambazo tunazifanya.
Kwa hiyo, Serikali inatambua ukubwa wa tatizo hili na inaweka uzito unaostahili na Mheshimiwa Rais tayari alishatuelekeza wasaidizi wake na sisi tunatembea kwenye nyayo zake kuhakikisha tunamaliza tatizo hilo la manung‟uniko ya askari.
Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo kwenye upande wa madai yao nimeelekeza kila ambaye anatunza kumbukumbu za askari waweze kuhakikisha kwamba wanaorodhesha vizuri kuwarahisishia wale wanaokagua, wanaofanya ukaguzi ili madai hayo ya askari yasikae muda mrefu sawasawa na maeneo mengine ambayo yana uficho ama yana tatizo la kuweza kufanya ukaguzi kwa sababu askari anapokuwa kazini huku anadai inampunguzia morali ya kazi na inampunguzia uwezo wake wa kufanya kazi.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nianze kuipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa ujenzi wa daraja la Igumbilo ambalo leo hii wakimbiza mwenge wanalizindua pale katika Jimbo la Iringa Mjini.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kuhusiana na ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami kutoka Dodoma - Mtera - Iringa ambao umekamilika lakini sasa kuna malori makubwa sana yanakatiza katikati ya mji na kusababisha msongamano na barabara hii kuharibika katikati ya mji. Ni lini sasa ule mchepuko ambao ulikuwa umetengwa, ambao unatokea kwenye Chuo cha Tumaini kwenda kwenye barabara kuu utakamilika kwa sababu sasa hivi magari mengi sana yanapita kwenye ile barabara? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kutoka Mkoa mzito wa Iringa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mchepuo wa Iringa upo katika mipango yetu. Naomba nimhakikishie kwamba kile ambacho wao kwa maana ya RCC walikileta kwetu na sisi tumekichukua, tutakifuatilia kuhakikisha kwamba tunakitekeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini? Naomba tu Mheshimiwa Mbunge anipe nafasi kwa sababu siyo sahihi sana kutamka tarehe hapa, lakini naomba aangalie dhamira yetu kwamba ni ya dhati na tutatekeleza mradi huo wa ujenzi wa mchepuo wa barabara pale Mjini Iringa.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa muda mrefu sana Serikali iliahidi kujenga barabara inayokwenda kwenye hifadhi la Ruaha National Park na nakumbuka nilishawahi kuleta swali hapa Bungeni na Mheshimiwa ambaye sasa hivi ni Rais alikuwa Waziri alijibu kwamba, kuna pesa zinatoka Marekani kwa ajili ya ujenzi wa hiyo barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba Mheshimiwa anijibu ni kwa nini, kwa sababu barabara hii ni muhimu sana kwenye Mkoa wetu wa Iringa.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba anijibu kwa sababu katika tengeo la bajeti ya safari hii sijaielewa vizuri, sasa atuambie ni lini barabara ile itajengwa inayokwenda kwenye Ruaha National Park?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, barabara hiyo hatujaiweka katika mwaka huu wa fedha unaoanza Julai, lakini namhakikishia ahadi hii kama ambavyo ilitolewa na Mheshimiwa Rais na viongozi wengine itatekelezwa kama ilivyoahidiwa kabla ya kipindi hiki tulichopewa cha uongozi kwisha.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kwa kuwa hili ni ombi, basi tunalichukua, halafu mimi na yeye tutakaa, tunajuana ma-comrade, tuweze kuona uwezekano wa kulitimza hilo.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali la nyongeza.
Kumekuwepo na wimbi kubwa sana la ujambazi ambalo linafanywa na hawa vijana wanaojulikana kama panya road ambao wamekuwa wakileta utata sana katika miji mikubwa na sasa hivi mpaka Iringa wameshatokea, Serikali ina mpango gani ama mkakati gani wa kuondoa ujambazi, hawa panya road kwa sababu ni vijana ambao nasikia wanafahamika kwenye mitaa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la panya road, ni kweli kulikuwa na kundi la vijana ambalo lilikuwa linafanya uhalifu. Lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Kabati kwamba Jeshi la Polisi limefanya kazi nzuri kudhibiti kundi la vijana hawa na nadhani Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kwamba kwa kipindi fulani sasa matukio hayo hayajitokezi na vijana hao wamedhibitiwa.
MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Naomba niulize maswali mawili madogo tu ya nyongeza.
Kwa kuwa ugonjwa huu wa fistula umeleta athari sana kwa wanawake wakiwemo hata wanawake wa Iringa pamoja na Njombe, kutokana hasa na ukosefu wa vifaa vya kujifungulia na miundombinu migumu sana ambayo wanawake wamekuwa hawavifikii hata vituo vya afya wala zahanati.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wanawake kwanza hawajifungulii majumbani na vifaa kuwepo katika zahanati na vituo vya afya hasa vilivyopo katika vijiji vyetu huko ndani kabisa?
Swali la pili, je, Serikali imebaini ni kwa kiasi gani wanawake wameathirika kutokana na ugonjwa huu wa fistula?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, niruhusu kwanza niseme jambo moja kwa ufupi kwamba ugonjwa wa fistula ni ugonjwa ambao unasababisha kuwepo kwa tundu lisilo la kawaida kati ya uke na kibofu cha mkojo au kati ya uke na njia ya kutolea haja kubwa.
Jambo la pili ambalo ningependa kulifafanua ni kwamba, ugonjwa huu hausababishwi na laana, kurogwa au mwanamke kutembea na wanaume wengi wakati wa ujauzito. Nimeona niliseme hili kwa sababu wanawake wengi wamekuwa ni wahanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali yake mawili ya nyongeza; kwamba tuna mikakati gani sasa ya kuhakikisha wanawake wanajifungulia katika vituo vya afya. Tulieleza wakati tunawasilisha bajeti yetu hapa, la kwanza ni kwamba tutaendelea kutoa elimu kwa wanawake wajawazito kuhakikisha wanahudhuria kliniki wakati wanapokuwa wajawazito na especially tutahamasisha wale wanawake wa kuanzia miezi miwili.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo tutalifanya ni kuhakikisha kwamba tunaweka huduma za upasuaji wa dharura katika vituo vya afya. Nimesikiliza michango ya Waheshimiwa Wabunge wakati wa mjadala huu ambao unaendelea wa bajeti ya Serikali hasa Wabunge wa chama changu, wanawake wa Chama cha Mapinduzi, wameongea kwa sauti kubwa sana kuhusu umuhimu wa kuboresha huduma za upasuaji wa dharura.
Kwa hiyo, nataka kumthibitishia Mheshimiwa Ritta Kabati kwamba bajeti ya Wizara ya Afya inayokuja itahakikisha tunaweka vichocheo vya kuwafanya wanawake wahudhurie kliniki na nilishasema, tutatoa vifaa vya kujifungulia kwa wanawake 500,000 kuanzia mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, madhara ya ugonjwa huu wa fistula. Yapo madhara ya kiafya, madhara ya kiuchumi na kijamii. Ya kiafya kama nilivyosema, mwanamke anatokwa na mkojo bila kujizuia, lakini pia haja kubwa inatoka katika njia ya uke. Kwa hiyo, hayo ni madhara ya kiafya na asilimia 85 ya wanawake ambao wanapata fistula wanapoteza watoto.
Mhehimiwa Naibu Spika, madhara makubwa ni ya kiuchumi na kijamii. Wanawake wengi wanaachwa na wanaume wao kwa sababu tu wamepata ugonjwa huo wa fistula, lakini wanawake hawa hawawezi kufanya shughuli za kujiletea maendeleo yao kwa sababu wana harufu, hawezi hata kufungua duka la maandazi au kigenge.
Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa ambalo nataka kuwathibitishia wanawake, ugonjwa wa fistula unatibika na matibabu yake yanapatikana katika hospitali zetu. Lengo la Wizara ya Afya ni kuhakikisha wanawake hawapati fistula, lakini kama wakipata basi wapate matibabu. Kwa hiyo, katika Hospitali zetu zote za Rufaa za Mikoa tutahakikisha huduma za upasuaji wa matibabu ya fistula zinapatikana. Nakushukuru.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo tu la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa TASAF III imekuwa ikihamasisha sana hizi kaya maskini kujiunga na Mfuko wa Bima za Jamii (CHF). Je, mpaka sasa ni kaya ngapi zimeweza kujiunga na huu Mfuko huu?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa tu niombe uniruhusu niweze kutoa maelezo ya utangulizi kidogo kabla sijajibu hoja yake. Kumekuwa na hoja na watu wengi wamekuwa wakitoa ushauri kwamba katika hizi kaya ambazo zinanufaika na ruzuku hii ya uhawilishaji, walazimishwe kujiunga na Mfuko wa Bima ya Afya ya Jamii.
Kwanza kabisa niseme duniani kote katika taratibu za uendeshaji wa mipango ya uhawilishaji wa fedha katika jamii huwa ni hiari. Kwa hiyo, tunachokifanya sisi kama TASAF ni kuhakikisha kwamba katika kila siku wanapoenda kupokea malipo tunawaelimisha kuhusiana na umuhimu wa kuweza kujiunga na Mfuko huu wa Bima ya Afya. Hadi sasa kaya 54,924 kutoka katika Halmashauri 28 zimeweza kujiunga na Mfuko huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tu pongezi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Chato ambayo zaidi ya 90% ya walengwa wake wameshajiunga na Mfuko wa Bima ya Afya. Nitoe pia pongezi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Liwale ambapo 60% ya walengwa wake tayari wameshajiunga na Mfuko wa Bima ya Afya.
Vilevile nitoe pongezi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Lindi, Halmashauri au Manispaa ya Mtwara pamoja na Kibaha lakini na nyingine nyingi. Niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge na ninyi pia mtusaidie kuendelea na uhamasishaji ili kuhakikisha kwamba walengwa hawa wanaweza kujiunga ili waweze kupata huduma ya matibabu ya afya pale wanapohitaji. Nakushukuru.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Naomba niulize maswali mawili tu ya nyongeza. Kwa kuwa Mkoa wa Iringa hasa katika Wilaya za Kilolo, Iringa Vijijini, Isimani, Kalenga na Mufindi, miradi mingi sana ya maji imekuwa haikamiliki kwa wakati na kusababisha wanawake wengi sana hata ndoa zao zimekuwa hatiani kwa sababu ya baridi; wamekuwa wakiamka asubuhi sana kwenda kutafuta maji. Je, ni lini sasa miradi ile iliyopo katika Mkoa wetu wa Iringa, Serikali itafanya kwa uharaka zaidi, pamoja na kuponya ndoa za wanawake wa Iringa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Wakandarasi wengi sana wamekuwa wakikamilisha miradi, lakini Serikali imekuwa haiwalipi madai yao kwa wakati. Je, ni mkakati gani umewekwa na Serikali kuhakikisha Wakandarasi hawa wanalipwa kwa wakati ili hii miradi iweze kukamilika kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba kutoa pole sana kwa wale ambao ndoa zao zimeingia hatiani, mashakani kwa hiyo changamoto ya maji. Naomba niwasihi akinababa kwamba hawa akinamama msiwahukumu katika hilo kwa sababu wanachokifanya ni kuwatafutia maji watoto na ninyi akinababa wenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la kwanza ni kwamba lini miradi hii itakamilika? Katika vipindi mbalimbali nimeelezea hapa, ni kweli miradi mingi ya maji imechelewa kukamilika kwa muda na watu mnafahamu ile miradi ya World Bank hasa tuliyokuwa tukiitekeleza katika kipindi kilichopita ambayo mpaka sasa tunaendelea nayo, ni kwamba miradi mingi Wakandarasi waliweza kutoa vifaa kutoka site, ni kwa sababu Wakandarasi wengi sana wali-raise certificate lakini walikuwa hawajalipwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa kama nilivyosema awali, ni kwamba, kwa sababu mwaka uliopita ulikuwa ni wenye changamoto kubwa sana, kwani fedha za miradi hazikwenda vizuri. Kama nilivyosema, katika Serikali hii ya Awamu ya Tano jukumu lake kubwa lilikuwa ni kukusanya kodi na mnafahamu kwamba tokea mwezi wa 12 mpaka hivi sasa, makusanyo ya kodi kila mwezi tumevunja rekodi ukilinganisha na kipindi kilichopita.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana certificate zote zilizokwenda katika Wizara ya Maji, zimelipwa na hata Naibu Waziri wa Maji juzi juzi hapa alikuwa anasema kwamba Mkandarasi yeyote mwenye certificate ambaye anatakiwa alipwe, afikishe haraka Wizara ya Maji pesa hizo zitalipwa. Ndiyo maana wale Wakandarasi wote waliokuwa hawajalipwa mwanzo, sasa hivi wote wamelipwa. Imani yetu kubwa ni kwamba sasa miradi hiyo itakwisha kwa sababu Wakandarasi wote wako site.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu madai yao kwamba ni lini yatalipwa? Ndicho nilichokisema hapa katika majibu yangu ya awali, kwamba sasa pesa zote za Wakandarasi wote zimeshapelekwa katika Halmashauri. Tunachohitaji ni kwamba zile certificate ambazo Wakandarasi wamelipa, Wakurugenzi wa Halmashauri wafanye haraka waweze kulipwa pesa zao ilimradi kwamba ile miradi iweze kukamilika na wananchi wetu waweze kupata huduma ya maji.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nataka kujua elimu shirikishi kuhusiana na wanafunzi wenye uhitaji maalum, kwa sababu shule yetu ya Lugalo iliyopo katika Mkoa wa Iringa ina wanafunzi ambao wana uhitaji maalum, lakini utakuta hawa wanafunzi hawana vifaa vya kujifunzia wala Walimu hawana vifaa vya kuwafundishia. Je, Serikali inasemaje kuhusiana na hilo?
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na elimu shirikishi na changamoto za elimu maalum, nadhani nimeeleza wazi dhamira ya Serikali ya kutatua changamoto zilizopo katika utoaji wa elimu kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mheshimiwa Ritta Kabati pengine anaona mikakati ambayo tumeiweka kwenye bajeti haitaweza kuondoa changamoto mahususi, ambazo ziko kwenye shule katika eneo lake, nimhakikishie kwamba, niko tayari kuongozana naye ili nione matatizo halisi ili tuweze kuyatatua, kwa sababu hiyo ndiyo dhamira ya Serikali.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo tu la nyongeza. Kwa kuwa, pamoja na mafunzo yanayotolewa kwa viongozi, wapo wanaokiuka taratibu za kuanzisha mashtaka katika utumishi wa umma, ikiwemo taratibu za uendeshaji wa mashauri ya nidhamu. Je, Waziri anatoa kauli gani kwa viongozi hao wasiotimiza wajibu wao?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati ambaye ametaka kusikia kauli ya Serikali tunasema nini kuhusiana na viongozi ambao wanakiuka taratibu katika uendeshaji wa masuala mbalimbali ya kinidhamu na uchukuaji wa hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitangulie kusema kwamba kumekuwa kuna kauli nyingi kwamba watumishi wa umma wanakatishwa tamaa, watumishi wa umma wanakosa kujiamini na mambo mengine kutokana na hatua mbalimbali za kinidhamu zinazochukuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba pamoja na malengo mbalimbali ya Serikali ya Awamu ya Tano, lengo mojawapo ni kuhakikisha kwamba tunarejesha nidhamu katika utumishi wa umma, ikiwemo pia kuchukua hatua kwa watumishi wa umma ambao watakiuka sheria, kanuni na taratibu. Endapo mtumishi wa umma yuko katika mstari anatekeleza wajibu wake ipasavyo, sioni ni kwa nini kuwe na hisia au hofu. Niwahakikishie tu kwamba, Serikali yao iko pamoja nao na hakuna ambaye ataonewa bila kufuata taratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tu kusema mambo yafuatayo:-
Taratibu nzima za kinidhamu zinasimamiwa na Sheria yenyewe ya Utumishi wa Umma, Kifungu cha 23(2), lakini kwa mujibu wa Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2003 kwa mujibu wa Kanuni ya 42, 47 na Kanuni nyinginezo, napenda kusema utaratibu mdogo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya hatua yoyote ya nidhamu haijachukuliwa ni lazima kuwe na hati ya mashtaka, ambapo mtuhumiwa au mtumishi huyo wa umma atapewa nafasi lakini vilevile katika hati hiyo atakuwa ameelezewa shutuma zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ni lazima mtumishi wa umma huyo anayetuhumiwa apate haki au fursa ya kuweza kujibu hati hiyo ya mashtaka ambayo amepatiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ni lazima iundwe Kamati huru ya uchunguzi ambayo itampa fursa pia mtuhumiwa aweze kujibu au kukanusha tuhuma zilizoko chini yake. Vilevile kwa mujibu wa Kanuni ya 47 Mtumishi huyu wa Umma anayetuhumiwa atakuwa na haki ya kusikilizwa kikamilifu, atakuwa na haki ya kuweza kumhoji mwajiri, atakuwa na haki ya kuweza kuona vielelezo mbalimbali vilivyotumiwa katika kumshtaki. Pia Kamati hii sasa ya Uchunguzi, ziko ambazo zimekuwa zikikiuka taratibu, ni lazima ndani ya siku 30 baada ya kutoa uamuzi wake iweze kuwasilisha ripoti katika mamlaka ya nidhamu na ajira. Baada ya siku 30 tangu ambapo Kamati ya Uchunguzi imewasilisha ripoti yake ni lazima mamlaka ya ajira iweze kumjulisha mtuhumiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, endapo mtuhumiwa atakuwa hajaarifiwa ndani ya siku husika, basi italazimika kuondolewa mashtaka na atakuwa huru kwa mujibu wa kifungu cha 48(9) cha Sheria ya Utumishi wa Umma. Nazitaka mamlaka mbalimbali za nidhamu kuhakikisha wanatimiza matakwa ya sheria hizi ili wasije wakawasababishia usumbufu watumishi wa umma vilevile wasije wakaisababishia Serikali hasara baadaye.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri.
Mheshimiwa Spika, kwa kweli katika Mkoa wetu wa Iringa tatizo hili limekuwa kubwa sana. Kwa mwaka 2016 tu zimeripotiwa karibu kesi 221 na kesi zilizopo Mahakamani zilizofikishwa ni 37 tu. Kwa kuwa kumekuwa na ukiritimba mkubwa sana wa kushughulikia hizi kesi, sasa kutokana na ukubwa wa tatizo hilo ni kwa nini Serikali isianzishe Mahakama Maalum ya kushughulikia kesi hizi yaani Sexual Offence Court kama wenzetu South Africa?
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa suala hili ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu kama ilivyo Mahakama ya Mafisadi, Mahakama ya Ardhi. Kama jambo hili ni gumu ni kwa nini kesi hizi zisipewe kipaumbele kama kesi za watu wenye ualbino? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa, hili tatizo kwa kweli limekuwa likiwaathiri sana watoto wanaobakwa, wazazi, hata sisi viongozi. Na kesi hizi zimekuwa zikichukua muda mrefu sana na kuathiri ushahidi mzima na mbaya zaidi hawa wenzetu wabakaji wamekuwa wakitumia wanasheria wanapopelekwa mahakamani, lakini hawa wenzetu ambao wamekuwa wakipata hizi kesi wamekuwa hawana uwezo, wengi hawana uwezo wa kuwatumia wanasheria.
Ni kwa nini, Serikali isiweke utaratibu wa kuwapatia msaada wa kisheria waathirika wa tatizo hili, badala ya kutegemea NGO ambazo nyingi haziko huko vijijini?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nikiri kabisa kwamba kuna tatizo kubwa siyo tu Iringa, lakini na sehemu zingine za Tanzania. Jana na juzi nilikuwa Mkoani Iringa kujiridhisha mimi mwenyewe kuhusu hali hiyo, nimefika mpaka magerezani.
Mheshimiwa Spika, kwa kweli kwa takwimu Kitaifa kwa miaka miwili mitatu iliyopita ni kwamba, kila siku ya Mungu kuna matukio 19 ya kubaka na kulawiti hapa Tanzania.
Mheshimiwa Spika, tatizo kubwa la matendo haya kwa upande wa Iringa ni kwamba yanatokea katika familia na ndugu, lakini familia hizo tunapopeleka kesi mahakamani ama tunapochunguza wanalindana, hawatoi ushirikiano kwa vyombo vyetu vya upelelezi ndiyo maana kesi nyingi zinachelewa. Hata tukianzisha mahakama hiyo ya Sexual Offences Court or whatever, bado hiyo mahakama itakwama kwa sababu wananchi hawajapata uelewa kwamba, wanavyolindana ndivyo wanazidi kuchochea hayo makosa.
Mheshimiwa Spika, namuomba Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote kutoka Mkoa wa Iringa akiwemo Mheshimiwa Msigwa na wengine, naomba tuendeshe kampeni kwa pamoja kuwaomba wananchi wetu, wapiga kura wetu, waachane na mchezo huu wa kulindana katika makosa haya. Otherwise Iringa baada ya muda si mrefu tutakuwa na idadi kubwa ya vijana waliokwishaharibika.
Mheshimiwa Spika, suala la kutoa msaada kwa waathirika hilo liko wazi na leo hii akisoma Mheshimiwa Mbunge Order Paper, nawasilisha hapa Muswada wa Msaada wa Kisheria. Sheria hiyo, nawahakikishia wananchi utawasaidia sana Watanzania, siyo tu waathirika wa vitendo hivi, lakini vilevile wajane, wanawake wanaonyanyaswa wakati wa mirathi, katika ndoa, katika talaka na kadhalika ili tuweze kukidhi matakwa ya Ibara ya 13 ya Katiba ya usawa kwa kila mtu mbele ya sheria. Ahsante.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru sana. Kwa kuwa barabara inayokwenda katika mbuga za wanyama katika Mkoa wetu wa Iringa ni barabara ya kiuchumi pia na Serikali kwa mara ya mwisho nilipouliza swali hilo iliniambia kwamba inafanya upembuzi yakinifu.
Je, ni lini sasa Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara hiyo kwa sababu hii barabara tunategemea kwamba kama itakuwa imemalizika, uchumi wa Iringa kutumia utalii utaongezeka?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Ritta Kabati pamoja na Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, walimchukua Waziri wangu wakaenda kuikagua barabara hii na nafahamu aliyowaahidi alipokuwa kule site.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikuhakikishie, yale ambayo Waziri wangu aliwaelezeni kule site ni lazima tutayatekeleza.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti,
ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko kwenye Kamati ya Miundombinu; kwa kuwa uwanja huo huo wa Nduli tayari kuna pesa zimetengwa kwa ajili ya ukarabati huo lakini pia mradi huu umeshakubaliwa na wananchi kwa sababu
Serikali tayari ilishakaa na wananchi waliopo katika eneo lile. Sasa naomba jibu kutoka kwa Serikali, kwa sababu kuna wananchi ambao wamekuwa wakiendeleza maeneo ambayo yataguswa sasa ni lini itaweka alama na ili
wasiyaendeleze maeneo yale ili wakati wa kulipa fidia pesa iwe kidogo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA
MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ritta Kabati amekuwa akihoji haya masuala ndani ya Kamati ya Miundombimu na mimi niendelee kumpongeza kwa namna anavyochukua hatua kuwatetea wananchi na kuhakikisha kwamba maslahi yao yanazingatiwa na Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu kama
ambavyo nimekuwa nikimhakikishia mara nyingi katika Vikao vya Kamati, kwamba kazi hii ya kuweka alama tutaifanya hivi karibuni. Naongelea si zaidi ya miezi mitatu, minne ijayo kazi hii itakuwa imekamilika ili kuhakikisha kwamba wananchi wa pale wanajua mipaka ya maeneo tutakayotumia katika kukarabati na kupanua ule uwanja wa Nduli.
MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo tu la nyongeza. Kwa kuwa huu udhalilishaji ambao umekuwa ukifanyika na hao wawekezaji siyo katika migodi tu, upo hata katika viwanda vyetu. Nimeshuhudia mara nyingi sana Mheshimiwa Naibu Waziri akienda kusuluhisha migogoro hasa ikihusiana na unyanyasaji wa wafanyakazi. Je, ni adhabu gani kubwa kabisa ambao wamekuwa wakipatiwa hawa waajiri au wawekezaji ambao wamekuwa wakiwanyanyasa hawa wafanyakazi. Kwa sababu nimeona jambo hili limekuwa likijirudia mara kwa mara.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI,VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, kila mwekezaji anayekuja kuwekeza hapa nchini hasa wale ambao wanapitia TIC na wale ambao wamejisajili katika Vyama vya Waajiri. Wamekuwa wakipewa sheria za nchi hii na utaratibu ambao unapaswa kufuatwa na jambo lolote linalojitokeza kinyume chake hapo sisi kama Serikali tumeendelea kuchukua hatua stahiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna changamoto kubwa sana kwa wawekezaji raia wa China ambao wengi wamekuwa wakiingia nchini na taratibu za kisheria zimekuwa hazifuatwi, lakini wale ambao wamesajiliwa wako chini ya ATE. ATE wamefanya kazi kubwa ya tafsiri sheria za kazi za nchi yetu kwenda katika lugha ya Kichina. Maana mwanzoni wao walikuwa wanatumia excuse ya kutofahamu sheria, ingawa katika principle zile za sheria katika ile maxim inayosema ignorantia juris non excusat, ambayo inasema muhimu kabisa kwamba hakuna excuse kwa mtu ambaye hafahamu sheria. Kwa hiyo walichokifanya hawa waajiri wametafsiri sheria zile, lakini bado kuna watu ambao wanakiuka taratibu hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tamko tu mbele ya Bunge hili kwamba wale waajiri wote hasa wawekezaji ambao wanafahamu sheria za nchi zetu, wanapaswa kufuata utaratibu ambao wanaendelea na unyanyasaji, tutaendelea kuwachukulia hatua stahiki ili kuhakikisha kwamba, tunaondoa dhana hii ya udhalilishaji na unyanyasaji wa wafanyakazi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia adhabu kubwa ambayo tumekuwa tukiichukua ni kwamba, tumekuwa tukiwandoa nchini mara moja wale wote ambao tunawabaini ni wageni wanawadhalilisha Watanzania katika nchi yetu ili tutengeneze kitu kinaitwa deterrence, mtu mwingine yeyote asiweze kurudia kosa hilo.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali moja tu dogo tu la nyongeza. Kwa kuwa, Mkoa wetu wa Iringa una mito kama Ruaha, Mto Lukosi na kadhalika, lakini wananchi wamekuwa wakipata shida sana kwa suala la maji hasa vijijini ikiwepo Kilolo na Mufindi. Ni kwa nini Serikali sasa isitumie mito hii kuondoa huu upungufu ambao upo katika Mkoa wetu wa Iringa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mkoa wa Iringa una utajiri mkubwa sana wa mito ikiwepo Ruaha Mkuu, lakini bado kuna Ruaha Mdogo, kuna Mto Lukosi ambao unatokea maeneo ya Kilolo. Kutokana na utajiri huo wa kuwa na mito mingi, kwanza kabisa Mto Ruaha Iringa Mjini tumeutumia, maji yanapatikana kwa asilimia 100 katika Mji wa Iringa. Sasa hivi tunaanza kusambaza maji kuyapeleka nje ya Mji wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutumia Mto Lukosi, nimeenda kule Kilolo, sasa hivi tunafanya utaratibu wa kuhakikisha tunasanifu mradi ili tuweze kutoa maji Mto Lukosi kuyapeleka maeneo yanayopitiwa na huo mto kuhakikisha kwamba maeneo mengi ya Iringa yanakuwa na maji ya kutosha ambayo ni safi na salama.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali tu madogo ya nyongeza. Kwa kuwa tumekuwa tukikaa katika vikao vya Bodi za Barabara mara nyingi sana hasa katika Mkoa wetu wa Iringa, barabara nyingi sana za Halmashauri zetu tunakuwa tukipeleka lakini hazipandishwi daraja. Je, ni vigezo gani sasa vinatumika maana utakuta sehemu nyingine barabara zinapandishwa lakini sehemu nyingine barabara nyingi hazipandishwi madaraja?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza pesa kwenye Halmashauri kwa sababu Halmashauri nyingi barabara zake ni mbovu sana ili Halmashauri hizi ziweze kutengeneza barabara zake kwa kiwango?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, vigezo vya kupandisha hadhi barabara vimeainishwa katika Sheria ya Barabara pamoja na Kanuni zake kama ambavyo nilisema katika jibu langu la swali la msingi. Vigezo hivyo havijabadilika na kama tutataka kubadilisha tutakuja Bungeni kuvibadilisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuongeza fedha; fedha nazo tumekubaliana kwamba Mfuko wa Barabara unagawa asilimia thelathini zinaenda kwenye Halmashauri na asilimia 70 zinaenda kuhudumia barabara za trunk road za mikoa. Sasa kama tunadhani kwamba formular hii kwa sasa labda haitufai bado ni suala la kuamua sisi Waheshimiwa Wabunge ndani ya Bunge hili Tukufu ili tuweze kubadilisha zile sheria ambazo tulikubaliana wenyewe.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, Mheshimiwa Waziri alipokuwa anajibu majibu yake alisema kwamba, kwenye miji mikubwa kuna hiyo huduma inatolewa, lakini ukija kwenye miji midogo kwa mfano Iringa kuna vijana wengi sana wameathirika. Lakini tumshukuru sana Dkt. Ngala pale Iringa, ameweza kuhamasisha wananchi wamefungua vituo kama hivi, lakini sasa wananchi wanashindwa gharama imekuwa kubwa sana kwenda kwenye vituo.
Sasa je, Serikali iko tayari kutoa ruzuku kwa watu ambao wamenzisha vituo hivi ili viweze kusaidia kwenye miji midogo kama Iringa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nijibu maswali haya mawili, Mheshimiwa Waziri wa Nchi atamalizia kwa ujumla yanayohusu supply reduction.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la kwanza la Mheshimiwa Amina Mollel, kwanza nimpongeze siku ya jana aliniletea wageni kutoka Chama cha Wananchi ambao wanajihusisha na Afya ya Akili Nchini na katika mazungumzo tuliyoyafanya ni pamoja na hili suala la Madaktari Bingwa wa Afya ya Akili kwenye Mikoa nchini. Mkakati tulionao na ndio taarifa niliyowapa wale wananchi wenzetu ni kwamba Serikali ina-scale up huu mkakati wa kuwa na hizi kliniki kama iliyopo Muhimbili, Temeke na Mwananyamala kwa mwaka huu kwenye mikoa kumi ya Tanzania Bara na kwa mwaka ujao tutaongeza mikoa mingine kumi, tunakwenda kwa awamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, kila tutakapoanzisha hii kliniki ya methadone ni lazima awepo Daktari Bingwa anayehusika na ku-administrate hiyo dawa kwa sababu methadone inalindwa kwa taratibu maalum za kuitunza na kuitoa kwa wagonjwa. Kwa hiyo, ni lazima awepo Daktari Bingwa anayeweza kufanya hivyo kwa hivyo, kwa mwaka huu nimhakikishie Mheshimiwa Amina Mollel kwamba tutakuwa na Madaktari Bingwa kwenye mikoa kumi ncjini, pindi kliniki za methadone zitakapoanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni la Mheshimia Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kuhusu hizi kliniki na rehabilitation centres kwenye Mikoa; kwa sasa kweli, tuko Dar es Salaam peke yake, lakini kwenye mkakati wetu tunakwenda kwenye mikoa kumi kama nilivyosema. Na kwenye kila kanda tunakwenda kuanzisha rehabilitation centre ambapo tutakuwanazo nne sasa katika nchji nzima. Kwa hivyo, hii ni mikakati ambayo tunayo katika siku za usoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ruzuku, Serikali haina utaratibu wa kutoa ruzuku kwenye taasisi mbalimbali za binafsi, kwa sababu wao wanafanya kwa hiyari na tunawaomba na kuwatia moyo waendelee kufanya hivyohivyo kwa hiyari, lakini sisi kama Serikali tuna mikakati yetu ya kuwasaidia wenzetu ambao wameathirika na dawa za kulevya.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ninaomba nijibu maswali ya nyongeza yaliyoulizwa kwa umoja wake, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwanza nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya, kwa majibu mazuri aliyokwishakuyatoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tena kwa kulipongeza Bunge letu Tukufu kwa sababu mwaka 2015, ndilo lililosababisha kufanyika kwa mageuzi makubwa ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini kwa kutungwa kwa sheria mpya ambayo imeunda hiyo mamlaka sasa ambayo tumemuona Kamishna Jenerali akifanya kazi kubwa sana kwa kushirikiana na makamishna wenzake kuhakikisha kwamba tunapambana na tatizo la dawa za kulevya nchini.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niliarifu Bunge
lako Tukufu Kamishna Jenerali baada ya kuteuliwa na mamlaka kuanza kazi rasmi, ameshahakikisha ametengeneza Mpango Mkakati Maalum wa Taifa wa kuhakikisha kwamba tatizo hili la dawa za kulevya nchini linaondoka. Na mpango mkakati huo unashirikisha pande zote mbili za Muungano, upande wa Zanzibar na upande wa huku Bara. Kwa hiyo, Mheshimiwa Khatib wala usiwe na wasiwasi, tunafanya kazi hizi kwa pamoja, vyombo hivi vyote viwili vinafanya kazi kwa pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumegundua kwamba, wenzetu wa private sector wanafanya kazi nzuri sana kwenye mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini. Na hivyo nichukue nafasi hii kwanza niwapongeze wale wote ambao wameamua kujitolea kusaidiana na Serikali katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania, tunawashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika mwaka huu wa bajeti, Ofisi ya Waziri Mkuu imeamua kuweka bajeti kidogo ambayo itasaidia kushirikiana na hao wenzetu ambao wameonesha kwamba, wana nia ama ya kuanzisha sobber houses kwa ajili ya kuwasaidia hawa walioathirika na dawa za kulevya, lakini vilevile kufanya kampeni na kuleta uhamasishaji mkubwa wa kuwasaidia vijana wetu kuwaondoa kwenye tatizo hili.
Kwa hiyo, tuko pamoja tunafanya kazi hii kwa pamoja, mapambano yanaendelea na tunataka kuona kwamba tunaondoa tatizo hili katika nchi yetu. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza na nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake. Pamoja na Serikali kukiri kuwa zao la mbao linachangia pato la Taifa kwa kiasi kikubwa nchini, lakini barabara zinazoingia katika maeneo ya misitu ni mbovu sana na hazipitiki hasa wakati wa mvua. Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka lami katika maeneo hayo ambako mbao hizo zinavunwa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa serikali imekuwa ikimuuzia mwekezaji wa nje (MPM Mgololo) nusu bei ya magogo, je, iko tayari sasa kuwauzia wajasiliamali wetu bei sawa na hiyo ili kuitikia wito wa uchumi wa viwanda. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Ritta kwanza kwa kuonesha nia na dhamira ya kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuendeleza viwanda nchini na hasa viwanda vinavyopata malighafi yake kupitia misitu; lakini pia nijibu maswali yake ya nyongeza mawili kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza la uboreshaji wa miundombinu ya barabara. Kwanza ni jambo ambalo hata upande wa Serikali ni la interest, kwamba maeneo ya mashamba yaweze kupitika kirahisi kwa ajili ya kuweza kuyahudumia mashamba yenyewe. Hata hivyo kuhusiana na suala la barabara zainazokwenda kwenye mashamba yenyewe ambazo zipo kimsingi chini ya Halmashauri ya Wilaya, barabara za makundi haya mawili zinashughulikiwa kwa namna tofauti.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi barabara ambazo zipo chini ya Halmashauri; katika Halmashauri ambazo zina mashamba Serikali inachokifanya ni kuweza kuchangia nguvu na uwezo wa kuweza kuhudumia barabara hizo kupitia uazimishaji wa mitambo mbalimbali ya ujenzi wa barabara. Mahali ambapo Serikali za Halmashauri zenyewe huweka mafuta kwenye mitambo hiyo na kuwezesha ujenzi wa barabara hizo. Serikali itaendelea kutumia njia hiyo ili kuweza kuhakikisha kwamba barabara hizo zinaendelea kuwa bora zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa barabara za ndani, tutaendelea kuziboresha kama ambavyo tunaendelea kufanya. Nimshauri tu Mheshimiwa Ritta kwamba haiwezekani kufanya barabara hizo zikafikia kiwango cha lami kwa sasa kwa sababu ya majukumu mengine ya Serikali ya uendelezaji wa miundombinu katika maeneo mengine, hizi za mashambani zitakuwa bora lakini katika kiwango hicho hicho cha barabara za udongo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la mwekezaji wa Kiwanda cha Karatasi pale Mgololo (MPM); suala hili ni pana, kubwa na la kina na Serikali mara kwa mara imekuwa ikitoa maelezo kuhusu suala hili la mwekezaji huyu ambaye historia yake ni ndefu inaanzia wakati wa Sera ya Ubinafsishaji ya Taifa huko miaka ya nyuma. Hata hivyo, kwa hali ilivyo sasa maelezo ninayoweza kuyatoa hapa kwa sasa hivi ni kwamba kwanza ieleweke kwamba miti ambayo ilikuwa inauzwa au ambayo inauzwa kwa mwekezaji ni magogo yanayotokana na miti ambayo ni ya umri mdogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, umri wa uvunaji wa miti
kwa ajili ya bidhaa ya mbao ni miaka 25 na zaidi, lakini magogo haya ambayo yanauzwa kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa ambayo inakwenda kuwa malighafi kwa ajili ya uzalishaji wa karatasi inayoitwa pulp ni miaka kuanzia 14.
Kwa hiyo, si magogo yale yale ambayo anauziwa mwekezaji huyu ambayo wanauziwa wazalishaji wa mbao katika maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa ninachoweza kusema ni kwamba, kwa sababu ya kina cha maelezo katika suala hili, Mheshimiwa Waziri ameandaa maelezo ya kutosha kwa kirefu kuhusiana na suala hili kwa sababu ya kupokea hoja mbalimbali kutoka kwa wananchi wa maeneo hayo hayo na Mheshimiwa Ritta Kabati kwa kuwa ameungana na wananchi wa maeneo hayo kutaka kujua ni namna gani wananchi wananufaika zaidi na Taifa linanufaika zaidi basi muipe fursa Serikali tuweze kupata nafasi Mheshimiwa Waziri atakuja kutoa maelezo ya kina zaidi katika wakati ambao ataweza kutoa maelekezo.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukurru sana. Naomba tu nimuulize Mheshimiwa Waziri maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nianze na kuipongeza Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa kuhakikisha kwamba kaya maskini angalau zinaweza kunufaika na huu mpango wa TASAF na kwa kweli katika mkoa wetu kaya nyingi zimeweza kunufaika na mpango huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa katika Manispaa yetu ya Iringa ambayo ipo Jimbo la Iringa Mjini tuna mitaa 192 na mitaa 98 tu ndiyo ambayo imeweza kunufaika na mpango huu na kuna mitaa 84 ambayo bado haijaweza kufikiwa kabisa na mpango huu wa TASAF; kwa mfano kwenye Kata ya Nduli kuna mitaa ya Kisoeyo, Mikoba, Kilimahewa, Mgongo na Njiapanda na kwenye Kata ya Kituli kuna mtaa wa Hoho; Kata ya Mkwawa kuna mtaa wa Mosi. Je, ni lini Serikali sasa itazifikia kaya hizi maana hali ya kaya katika mitaa hii ni mbaya kuliko hata zile ambazo zimeweza kufikiwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nina swali lingine la pili. Kwa kuwa zipo kaya ambazo ni maskini na pia zina watoto wenye ulemavu. Kwa mfano katika Mkoa wetu wa Iringa kwenye Jimbo la Kilolo, Kijiji cha Lulanzi, kuna kaya ambayo ina watoto wanne, wote wana ulemavu na baba yao amepooza, mama yao sasa hivi amevunjika mguu. Je, katika mpango huu Serikali inawasaidiaje watu ambao tayari ni maskini na hawawezi kufanya kitu chochote katika kuwasaidia ili waweze kupata miradi? Kwa mfano labda kujengewa/kuwekewa mradi wa kisima ambao wanaweza wakauza maji wakiwa pale pale au wakapewa bajaji ili kuweza kunusuru kaya ambazo ni walemavu halafu ni maskini?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa niseme Serikali inakubali kwamba ni kweli si vijiji vyote, mitaa, kata na shehia nchini mwetu zimeweza kufikiwa na mpango huu wa TASAF. Ni takriban asilimia 70 tu kama nilivyoeleza ya vijiji, kata, shehia 9,989 ndiyo imefikiwa.
Napenda tu kumweleza Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi sasa tumeanza taratibu, tunasubiri tu fedha zitakapotoka tuweze kuendelea na zoezi la kuwatambua na kuwaandikisha walengwa liweze kufanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia sasa hivi tuko katika mpango tuliokuwa tunamalizia kipindi cha kwanza cha awamu ya tatu ya TASAf ambayo itamalizika mwaka 2018 kuelekea 2019; na sasa hivi tumeanza kusanifu awamu nyingine na tunaamini pia katika zoezi hilo nalo pia tutaendelea kufanya utambuzi na kujua program itakuwaje.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba pindi tu fedha zitakapopatikana tutaweza kuendelea na zoezi la utambuzi wa walengwa na kuweza kuwaandikisha. Vile vile tutakapoendelea katika kipindi cha pili cha awamu ya tatu ya TASAF tunaamini walengwa wataweza kunufaika.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili amezungumzia kaya za watu ambao ni maskini ambao unakuta ni watu wenye ulemavu. Nipende tu kumweleza Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati program hii ya TASAF awamu ya tatu inasanifiwa, suala zima la ulemavu halikuwa kigezo, kigezo kilikuwa ni umaskini lakini pia walikuwa wanaangalia umaskini wa kaya nzima kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika aina za ruzuku ambazo zinatolewa, ruzuku ya kwanza kabisa ambayo inatolewa bila hata masharti ya kuangalia kama familia ina watoto ilikuwa inatolewa kwa kaya nzima. Hata hivyo, nipende kusema, endapo kaya hiyo ina watu wenye ulemavu ambao wako chini ya miaka minane walikuwa wanakuwa treated au wanahesabiwa kama watoto wengine katika familia hiyo kwa mujibu wa ruzuku.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa familia ambazo tumezikuta zina ulemavu wamekuwa wakishirikishwa katika miradi mbalimbali ya ajira ya muda. Hata hivyo, bado kama alivyoeleza yeye tulipata changamoto, ziko familia ambazo unakuta zina watu ambao wamezidi miaka 18, hata wakipewa ajira ya muda wengine ni mpaka wabebwe na hawawezi kufikia katika hiyo miradi mbalimbali. Niseme tu, tumelipokea na sasa hivi tunaposanifu awamu ya tatu ya mradi huu tutaendelea kuliangalia; kwamba katika awamu nyingine ni nini kifanyike kwa ajili ya watu wenye ulemavu lakini pia kwa sasa tunaangalia tunaweza tukawasaidiaje. Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake, naomba kuuliza maswali tu madogo ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa jibu katika swali langu la msingi linakiri kuwa kumbukumbu na hukumu katika Mahakama za Wilaya hadi Mahakama ya Rufani ni kwa Kiingereza. Je, Serikali haioni kuwa kumbukumbu na hukumu katika lugha ya kigeni yaani Kiingereza ni kikwazo kikubwa kwa mwananchi anayetaka kukata rufaa kwa kupata haki yake?
Swali la pili, kwa kuwa kauli mbiu ya Serikali ni haki sawa kwa wote na kwa wakati, lakini tumekuwa tukishuhudia Mahakama zikijitahidi kumaliza kesi zake, lakini hukumu zinakuwa zinapatikana kwa kuchelewa sana, hali inayopelekea wengine kutokukata rufaa kwa wakati na walioko gerezani kuendelea kuteseka gerezani.
Je, Serikali inatoa kauli gani? (Makofi)
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kukubaliana na Mheshimiwa Ritta Kabati kwamba ana hoja ya msingi, lakini nikumbushe tu Waheshimiwa Wabunge wote kwamba tuliamua mwaka 1964 kukifanya Kiswahili kuwa lugha ya Taifa, vilevile Kiingereza kuwa lugha ambayo tunaitumia katika shughuli za Serikali. Ni kama Mheshimiwa Baba wa Taifa alivyosema kwamba Kiingereza ndiyo Kiswahili cha dunia.
Kutoka 1964 mpaka sasa tumeweza kufanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha kwamba tunakiingiza Kiswahili katika mfumo wa Mahakama bila kupotosha utoaji haki.
Mheshimiwa Spika, kwanza ni suala la utumiaji wa Kiswahili kwa kumbukumbu, kwa hukumu, kwa uendeshaji katika Mahakama za Mwanzo ambao umefanikiwa sana. Hatujaona kabisa miscarriage of justice pale.
Mheshimiwa Spika, pili Taasisi ya Taaluma za Kiswahili (TATAKI) ambayo mwanzoni ilikuwa inaitwa TUKI (Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili) chini ya Profesa Mlacha, iliweza kushirikisha Baraza la Kiswahili la Tanzania pamoja na Wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wa Sheria, nilikuwepo mimi pamoja na Marehemu Profesa Joan Mwaikyusa, Mungu aiweke roho yake pema, peponi, tukaweza kutoa Kamusi ya kwanza ya Kiswahili ya Kisheria, yote haya ni maandalizi.
Mheshimiwa Spika, tatu, kila Muswada wa Sheria leo hii ukiletwa hapa Bungeni na sheria zenyewe, lazima ije kwa Kiingereza na Kiswahili na hilo wewe mwenyewe umekuwa ukisisitiza sana.
Mwisho BAKITA imeshakusanya sasa hivi Istilahi zaidi ya 200 za kisheria ambazo zinasubiri tu kusanifishwa (standardize). Kwa msingi huo, Mahakama yetu ambayo ni chombo huru katika Katiba yetu ni Muhimili unaojitegemea, una msingi sawa wa kutosha tuweze kupanua wigo wa matumizi ya Kiswahili katika kumbukumbu na hata kutoa hukumu hata kwenda Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi kwa kuanzia.
Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Kabati kwamba tunachoepusha hapa ni kukurupuka tu kuingia na kutumia Kiswahili ilikuwa tu ni kuepusha utata katika nyaraka zetu, ambiguities na kuwa equivocal, kuwa na utata katika utafsiri nyaraka za Kimahakama, ndiyo maana tumekwenda polepole sana.
Mheshimiwa Spika, suala la pili, nakubaliana naye kwa kweli haki iliyocheleweshwa ni haki iliyonyimwa, lakini ni kweli vilevile kuwa haki iliyowahishwa sana mara nyingi hukosa umakini. Kesi nyingi zinachelewa hasa za jinai kumalizika si kwa sababu ya Mahakama lakini kutokana na mchakato mzima wa utoaji haki. Kwa mfano, suala la upelelezi huchukua muda mrefu sana, na inachukua muda mrefu si kwa sababu vyombo vyetu vya dola havifanyi kazi, lakini kuna tatizo la kutopata ushirikiano mzuri kwa mashahidi mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, Iringa anakotoka Mheshimiwa Kabati, tuna kesi nyingi sana, sana za makosa ya kujamiiana na yanatokea ndani ya familia, kupata ushahidi mle ndani ni kazi kubwa kweli na ndiyo maana tunatoa wito kwa wananchi wote kushirikiana na vyombo vya dola pale inapotokea kosa, kusaidia katika ushahidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la kwamba, uthibitisho wa makosa mengine unahitaji Mkemia Mkuu achunguze na atoe jibu, inachukua muda mrefu, Mkemia Mkuu anaweza kuwa na mafaili 3000 ya uchunguzi na yote yanahitaji kwenda Mahakamani, kwa hiyo kazi ni kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na la mwisho ni uhitaji wa kisheria kwamba kila kosa lazima lithibitishwe beyond reasonable doubt yaani pasipo na wasiwasi wowote. Sasa hiyo hatuwezi kulikwepa ili kuweza kulinda haki za kila mtu.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa swali la msingi linafanana kabisa na tatizo tulilonalo katika Hospitali yetu ya Mkoa, karibu asilimia 85 ya Madaktari wa Hospitali ya Mkoa wa Iringa wanaishi nje kabisa ya hospitali ile na kusababisha wagonjwa kupata matatizo makubwa wanapokuja usiku kwa ajili ya matibabu. Tatizo kubwa lililoko katika Hospitali ya Mkoa kuna mwingiliano wa Magereza na Hospitali. Tulishauri mara nyingi kwamba Waziri wetu wa Afya pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani waweze kukaa pamoja waone kwamba lile gereza liweze kutoka ili madaktari wengi waweze kukaa karibu na Hospitali ile ya Mkoa ili kusaidia wagonjwa wanaofika hata usiku.
Je, ni lini sasa ombi hilo la Mkoa litaweza kutekelezeka ili wananchi wa Iringa waweze kupata haki ya kupata madaktari wakati wote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Kabati kwa sababu wiki mbili zilizopita tulikuwa pale Iringa tukaenda mpaka Kilolo na miongoni mwa mambo tuliyopitia katika sekta ya afya kipindi cha nyuma tulifika mpaka Hospitali ya Frelimo kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma. Kwa jambo hili, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa sababu Waziri wa Afya na Waziri wa Mambo ya Ndani wameshakaa tayari ku-discuss jambo hilo, usihofu kila kitu kitaenda vizuri lengo kubwa ni tuweze kuwapatia huduma wananchi wetu vizuri. Kwa hiyo, hilo jambo ondoa hofu kila kitu kitaenda vizuri Serikali itashughulikia.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali dogo tu la nyongeza.
Kwa kuwa uhaba wa Maafisa Ugani uko sawasawa kabisa na uhaba wa wataalam wa mifugo. Je, Serikali ina mpango gani wa kuajiri Maafisa Mifugo wa kutosha ili wananchi wasaidiwe haki katika Halmashauri zetu?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itashughulikia tatizo la uhaba wa Maafisa Ugani sambamba na tatizo la Maafisa wa Mifugo.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo mawili na nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake.
Je, Serikali inasaidiaje kufuatilia wafanyakazi wahamiaji nchi za Uarabuni na kwingineko ambako wanateseka bila kuridhia mkataba huo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa tumekuwa tukishuhudia baadhi ya watu ambao wamekuwa wakitafutiwa kazi kupitia hizi wakala za ajira (Employment Agency), lakini kumekuwa na malalamiko ya kupunjwa haki zao.
Je, Serikali inachukua hatua gani ili kulinda haki za wafanyakazi ambao wanapata ajira zao kupitia wakala hawa, pamoja na madalali ambao wamekuwa wakiwatafutia wafanyakazi wa majumbani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, kama nilivyosema katika majibu yangu ya msingi ya kwamba tuendelee kuangalia mazingira bora ya namna ya ku-ratify mkataba huu hasa pale ambapo kama nchi tutakuwa tumejiridhisha kwamba, mazingira ni rafiki na hivyo kuusaini mkataba huo ambao utasaidia sana katika kulinda haki za wafanyakazi wa ndani, lakini vilevile ambao wanatoka nje ya nchi, kwa maana ya Watanzania.
Mhweshimiwa Mwenyekiti, la pili la kuhusu Wakala wa Ajira; kama nilivyokuwa nikijibu katika maswali mengine ambayo yamewahi kuulizwa katika eneo hili, ni kwamba pale katika Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Kazi, Vijana na Ajira, ipo taasisi ambayo inashughulikia masuala ya ajira kwa maana ya wakala wa ajira ambaye anaitwa TaESA. Na rai yetu ilikuwa ni kwamba, wafanyakazi wote wa kitanzania ambao wanakwenda kufanya kazi nje ya nchi ni lazima wapitie TaESA, ili tuwatambue tujue na katika nchi ambazo wanakwenda. Tumefanya hivyo kwa sababu wakienda katika njia ambazo si sahihi, sisi kama Wizara si rahisi sana kuweza kufahamu akina nani wako wapi na ndio maana tunawataka kwamba wote wapitie katika ofisi zetu na sisi huwa tunaongea na Balozi husika, ili waweze kushughulikiwa matatizo pale wanapopatwa na matatizo nje ya nchi, ikiwemo ukosefu wa mikataba na haki nyingine.
MHE. RITTA A. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi kuuliza maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kuna baadhi ya wazazi au walezi hasa katika Majiji kwa mfano Jiji la Dar es Salaam wamekuwa wakiwatumia watoto wadogo kuomba omba hata kule kwenye magari, tumekuwa tukishuhudia na nimeona katika jibu la msingi Mheshimiwa Waziri amesema kwamba wazazi kama hao wanatakiwa wachukuliwe sheria/ hatua, kwa sababu watoto hawa wanakosa haki yao ya msingi na wakati elimu ni bila malipo.
Je, ni nani sasa anawachukulia hatua wale wazazi au walezi ambao wanawatumia watoto katika kuomba omba kwenye magari?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto ya mwaka 2008 mtoto hana haki zake kama tano. Mtoto ana haki ya kuishi, kuendelezwa, kulindwa, kushirikishwa na pia mtoto hana haki ya kutobaguliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba mtoto kama nilivyoainisha katika haki zake za msingi, ni jukumu la kwetu sisi wazazi, walezi, jamii na Serikali katika ngazi ya Mitaa na Serikali Kuu kuhakikisha kwamba mtoto anapata haki zake zote hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kabati alikuwa ameelekeza swali lake katika Mkoa wa Dar es Salaam, tuna mikakati mbalimbali ambayo tunaendelea nayo kuhakikisha kwamba watoto wale wa mitaani wanapata haki zao stahili pamoja na kuondolewa katika mitaa.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo tu mawili ya nyongeza.
Kwanza nikushukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yako, ningependa kujua tofauti kati ya hizi Mahakama za kawaida na Mahakama za Coroner?
Swali la pili, kwa kuwa hata katika Mkoa wetu wa Iringa, vipo vifo ambavyo huwa vinatokea vyenye utata; je, ni vifo vingapi ambavyo vilipelekea kuundwa hii Mahakama ya Coroner?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ipo tofauti kati ya Mahakama ya Coroner na Mahakama za kawaida za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya.
Kwanza kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, Mahakama ya Coroner kazi yake kubwa ni kupata chanzo cha kifo ambacho kimetokea na kina utata, kujua chanzo chake ni nini. Kwa hiyo, hiyo ndiyo kazi kubwa Mahakama ya Uchunguzi inafanywa ikiongozwa na Coroner na ndipo hapo unakuta atatumia madaktari, ma-pathologist, forensic experts, criminologist waweze kumsaidia kujua chanzo cha hicho kifo ni nini.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama ya Wilaya, wao wanakwenda mbele zaidi, wakishapata tukio kwamba limetokea wao sasa wanaangalia vilevile dhamira ya yule aliyetenda hilo kosa.
Mheshimiwa Naibu Spika, wewe mwenyewe ni Mwanasheria na kwa Waheshimiwa Wabunge ambao ni Wanasheria pia wataelewa lakini naomba nieleze tu kwamba Mahakama za Hakimu Mkazi, wao wanaongozwa na Kanuni ya Sheria inayosema tendo pekee halitoshi kuweza kumhukumu mtu, lazima liendane na dhamira ovu ya yule aliyetenda, yaani the act alone haitoshi it must be accompanied by blameworthy state of mind na kwa kilatini mnakumbuka mliosoma sheria „actus non facit reum nisi mens sit rea; kitendo pekee hakitoshi. Kwa hiyo, Mahakama ya Hakimu Mkazi kazi yake ni kuangalia kitendo kiendane vievile na dhamira ovu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kuhusu swali la pili la matukio yaliyotokea na kwa nini iliundwa hiyo Mahakama. Mheshimiwa naomba tu nikiri kwamba naliona tatizo la elimu kwa umma hapa, kwamba haijatosha na ndiyo maana pengine huduma hii ya Coroner naona Watanzania wengi hawajaielewa sana. Hili naliona ni tatizo ambalo Wizara yangu sasa nafikiri tutalikazania sana katika kipindi hiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba mashauri yanayopelekwa kwa Coroner au kwenye Mahakama hizi yapo, nakumbuka shauri moja ambalo mimi mwenyewe nilihusika ni Shauri Na. 152 la mwaka 2003, lilitokea Mbeya ambapo Mahakama ya Hakimu Mkazi ilikaa chini ya Coroner ya kuweza kupata ufumbuzi wa kitu kilichotokea katika Kituo cha Polisi na matokeo yake yalikuwa mazuri. Ndiyo maana nimesema kwa kweli ni wajibu wa Wizara hii sasa kuuelewesha umma vizuri zaidi kuhusu huduma hii ambayo ipo na hata muuliza swali wa kwanza alidhani kwamba hii mahakama haipo ni huduma ambayo tunafikiria kuianzisha.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza swali dogo tu la nyongeza. Kwa kuwa Hospitali yetu ya Manispaa ya Iringa ilifunguliwa ili kupunguza msongamano mkubwa sana uliopo katika Hospitali ya Mkoa, lakini mpaka leo hii Hopsitali hii haina mashine ya X-Ray wala Ultra Sound. Pia hospitali hii imekuwa ikihudumia mpaka wagonjwa wanaotoka Kilolo kwa sababu Kilolo pia Hospitali yao ya Wilaya imekaa vibaya kiasi kwamba wagonjwa wanaotoka kule Kilolo wanakuja kuhudumiwa katika hospitali hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kwamba, kama mashine hizi zingekuwepo zingeweza pia kuingiza pesa ili kuzisaidia ziweze kujiendesha. Je, Serikali sasa inaisaidiaje hospitali hii iweze kupata hizi mashine ili iweze kuhudumia wananchi waliopo katika Manispaa ya Iringa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nasema ngoja nilichukue hili kwa sababu katika kuangalia kwa haraka haraka sikuweza kufahamu kwamba mpaka hivi vifaa vya X-Ray bado vina changamoto kubwa, lakini naomba tulichukue hili kwa ajili ya kulifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitembelea kule Kilolo, nilijua kwamba watu wa Kilolo wote wanakuja kupata huduma pale na nilijua kwamba vifaa vyote vimekamilika. Jambo hili tutalifanyia kazi kwa pamoja ili Hospitali hii ya Manispaa iweze kutoa huduma bora kwa wananchi wote kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niseme kwamba tutashirikiana kwa pamoja na Mheshimiwa Ritta Kabati pamoja na Wabunge wengine wa huko ili hospitali ile ambayo ni centre kubwa sana ya magari makubwa yanayopita kutoka nchi za jirani kuja Tanzania iwe na uwezo wa kuwahudumia watu kwa kiwango kikubwa.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali madogo ya nyongeza. Kwanza kabisa nianze kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa mapokezi makubwa kabisa ya ndege ya Bombadier ambayo jana ilitua na Mheshimiwa Rais akiwa anaongoza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili pia niipongeze Serikali kwa kuanza sasa kujenga kiwanja chetu cha Nduli kwa sababu nina imani kabisa sasa hata utalii utafunguka katika Mkoa wetu wa Iringa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ndege ya Bombadier ina uwezo wa kutua katika kiwanja chenye urefu wa kilometa 1.2 na kiwanja chetu cha Nduli kina urefu wa kilometa 1.6, tatizo ni kipande tu kidogo cha mita kama 100 ambacho ni kibovu sana ambacho hakiwezi ndege kubwa kutua na hata zile ndege ndogo ambazo zinatua, zinatua kwa matatizo makubwa sana na mpaka sasa hivi kiwanja chetu kina abiria karibu 20,886,000. Je, Serikali sasa haioni umuhimu sasa wa kujenga hicho kipande kidogo cha mita 100 ili tuweze kupata ndege kubwa na hizo ndogo zipate kutua vizuri wakati tunasubiri huo ujenzi wa kiwanja hicho, kwa ufadhili wa Benki ya Dunia? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; nimesikia tayari zoezi la uthamini wa mali limeshaanza katika kiwanja chetu cha Nduli. Hofu yangu kubwa ni kwamba zoezi hili huwa linafanyika mapema kabisa lakini huwa linachukua muda mrefu sana kwa wananchi kulipwa mali zao, nina mfano halisi kabisa wa kiwanja cha ndege cha Songea ambacho toka mwaka 2010 karibu miaka nane bado hawajalipwa na vilevile hata barabara yetu ile ya mchepuo ilichukua karibu miaka sita mpaka wananchi kuanza kulipwa. Je, Serikali imejipangaje kuhakikisha kuwa wananchi hawa ambao wanapisha hiki kiwanja wanalipwa mapema zaidi? Mheshimiwa Naibu Sika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nizipokee pongezi nyingi ambazo amezitoa kwa kupokea ndege ambayo jana Mheshimiwa Rais ameipokea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia uboreshaji wa kiwanja hiki, amekuwa akifuatilia na mimi binafsi nilifika kuona hali ya uwanja. Suala la kwanza ambalo amelizungumzia juu ya kuongeza urefu wa kiwanja. Ilikuwa imetengwa shilingi bilioni 47 kwa ajili ya upanuzi wa kiwanja hiki lakini kwa bahati nzuri tumepata fedha kwa udhamini wa Benki ya Dunia tutakwenda kujenga kwa thamani ya shilingi bilioni 94.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii inaonesha kwamba huduma nyingi katika uwanja huu zitakuwa zimeongezeka. Hii ni pamoja na kuweka taa za kuongozea ndege, kuongeza urefu wa uwanja na sasa huu uwanja pamoja na taa zitakapowekwa utakuwa na urefu wa mita 2,500 kwa maana utaweza kumudu kiwango hiki ambacho Mheshimiwa Mbunge anaomba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Mbunge, wananchi wa Iringa na Watanzania kwa ujumla tuvute subira, tunaenda kuboresha huu uwanja utakwenda kuwa wa kisasa pamoja na kuweka majengo, jengo la abiria pamoja na jengo la wafanyakazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni ushahidi tosha kwamba sasa hivi compensation hazichelewi kulipwa. Viko viwanja ambavyo vinaendelea kujengwa kule Shinyanga, compensation imelipwa lakini uthamini umeshakamilika, tunaendelea kuhakiki wenzetu wa Wizara ya Fedha wanahakiki umethaminishwa kama Sh.3,043,626,000 kwa ajili ya kulipa compensation. Nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge uvute subira, uhakiki unafanyika na mara uhakiki ukikamilika fedha hizi zitalipwa kwa wananchi. Kwa hiyo, wananchi wasubiri kulipwa compensation yao. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naishukuru Serikali kwamba hii Awamu ya Tano imeagiza kwamba hii mifuko ya hifadhi ya jamii iweze kuwekeza katika viwanda na katika hivi vyama vya ushirika.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru pia Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wetu, alipokuja Mkoani Iringa katika ziara yake, alitembelea kile kinu chetu cha National Milling na aliahidi kwamba NSSF ingeweza kutoa mtaji ili kiweze kufanya kazi vizuri, pamoja na kutoa ajira nyingi kwa wananchi wa Iringa. Sasa nataka tu kujua: Je, agizo lake lile limeshafanyiaka? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza niendelee kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jinsi anavyojibu maswali ya Waheshimiwa Wabunge vizuri sana ndani ya Bunge lako la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba nchi yetu inaingia katika uchumi wa viwanda na hivyo basi Serikali kwa makusudi mazima imeiagiza Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ianze sasa kuhakikisha na yenyewe inaunga mkono nguvu za Serikali na mpango wa maendeleo wa Serikali wa kuingiza nchi yetu kwenye uchumi wa viwanda kwa kuhakikisha wanafufua baadhi ya viwanda ambavyo vilikuwa vimekufa na kuanzisha viwanda vingine vipya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana dada yangu, Mheshimiwa Rita Kabati, kwa karibu sana amefanya kazi na Serikali kwa kupitia Mfuko wa NSSF kuhakikisha kinu cha National Milling pale Iringa kinafufuliwa na kinafanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimthibitishie Mheshimiwa Dada Ritta Kabati kwamba NSSF kwa kushirikiana na Bodi ya Mazao Mchanganyiko wameshafikia hatua nzuri ya ununuzi wa mashine na vifaa vinavyotakiwa katika kufufua kinu chetu cha Iringa. Baada ya muda siyo mrefu, uzalishaji utaanza kwa nguvu sana na ajira zitaongezeka na hivyo basi, wananchi wa Mkoa wa Iringa na Mji wa Iringa wajue kwamba Mbunge wao amefanya kazi nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kushirikiana na Serikali na Mfuko wetu wa NSSF na Mifuko mingine ya Hifadhi ya Jamii, tuna mpango wa kufungua viwanda visivyopungua 25 na kuongeza idadi ya ajira zisizopungua 200,000 katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali. Kwanza niipongeze Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri ambayo imekuwa ikiifanya katika nchi hii. Hivi karibuni kulikuwepo na zoezi la uhakiki wa vyeti feki na katika uhakiki huo kuligundulika kwamba kuna vyeti feki katika taasisi nyingi na kusababisha sasa kuwepo na upungufu mkubwa sana katika taasisi mbalimbali na hasa katika hospitali zetu na Halmashauri zetu. Sasa napenda kujua je, ni lini sasa zoezi la kuziba zile nafasi ambazo wale wenye vyeti feki wameondolewa zitaweza kuzibwa ili kusaidia wale wafanyakazi waliopo wasifanye kazi kwenye mazingira magumu sana? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia ustawi wa watumishi lakini pia kwa namna ambavyo anafuatilia upungufu huu uliojitokeza wa watumishi kutokana na zoezi lililoendeshwa la wenye vyeti feki.
Mheshimiwa Spika, nipende tu kusema kwamba, tumekuwa tukieleza humu ndani tayari kibali kimeshatolewa cha ajira 15,000. Tulikuwa tunafanya mashauriano na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, wameshatuletea orodha maana yake ilikuwa ni lazima tujue katika kila kituo ni nafasi ipi ambayo iko wazi.
Mheshimiwa Spika, nipende tu kusema kwamba katika maeneo ambayo yameathirika sana ni sekta ya elimu pamoja na sekta ya afya kwa zaidi ya asilimia 70 na zaidi kidogo. Pia kwa sekta ya afya tu peke yake zaidi ya watumishi 3,360 wamekumbwa katika zoezi hili. Nimweleze tu kwamba tayari tumeshaanza mchakato huo na muda si mrefu nafasi hizo zitazibwa.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo tu la nyongeza japokuwa kidogo linafanana na muuliza swali aliyepita. Ili kurahisisha ukusanyaji na ulipaji kodi ni kwa nini TRA isiweke vituo katika kila Halmashauri ya Wilaya ili kupunguza usumbufu mkubwa wanaopata walipa kodi? Kwa mfano, ukichukulia Mkoa wetu wa Iringa, jiografia yake ni mbaya sana inawasabisha hata watu wengine kukwepa kodi kwa sababu tu vituo vya TRA viko mbali sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi na hakuna Taifa lolote linaweza kuendelea bila kukusanya mapato, tunafahamu kabisa hilo kama Wizara yenye mamlaka ya ukusanyaji wa mapato Tanzania. Hili la kuanzisha ofisi kila Halmashauri, nilishawahi kujibu ndani ya Bunge lako Tukufu kwamba kuanzishwa kwa ofisi huwa kuna tathmini ambayo huwa inafanyika kuangalia cost and benefit analysis ya kuanzisha ofisi hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikia Mheshimiwa Mbunge, tutafanya uhakiki na tathmini hiyo kujua kama kuna uhitaji mkubwa wa kuweka ofisi hizi katika kila Halmashauri ndani ya Mkoa wa Iringa.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona na kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, mwuliza swali alikuwa anauliza kuhusu ukarabati wa kituo, lakini kwa kuwa Wilaya ya Kilolo ni ya siku nyingi sana na haijawahi kujengewa Makao Makuu ya OCD yalipo Makao Makuu ya Wilaya toka imeanzishwa, na kufanya OCD kukaa mbali na DC. (Makofi)
Je, ni lini sasa Serikali itaona umuhimu wa kujenga Makao Makuu ya Polisi yalipo Makao Makuu ya Wilaya ya Kilolo?
NAIBU WAZIRI MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Spika, ni sahihi kabisa, Kilolo hatuna Kituo cha Polisi cha Wilaya na hii ni moja ya vituo 65 vya wilaya nchini ambavyo hatunavyo na ambavyo vipo katika mpango wa Serikali wa kuvijenga. Kwa hiyo, Kilolo ni kimojawapo.
Mheshimiwa Spika, wakati jitihada hizi za Serikali za kuweza kuona jinsi gani tunafanya kujenga vituo 65 zinaendelea, basi nataka nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya ziara katika Mkoa wa Iringa hivi karibuni ili tushirikiane tuangalie namna gani nyingine ambayo tunaweza tukafanya ili kuweza kuunga mkono jitihada za Serikali za kujenga kwa kushirikisha wadau mbalimbali.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pia nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Hospitali yetu ya Wilaya iliyopo katika Manispaa ya Iringa ilifunguliwa ili kupunguza msongamano mkubwa uliyopo katika hospitali ya mkoa, lakini hospitali ile mpaka sasa hivi haina jengo la vipimo, haina wodi za wagonjwa wengine ina wodi za wazazi na hospitali ile imekuwa ikisaidia wagonjwa wanaotoka katika Wilaya ya Kilolo, Iringa DC na kwingineko; na Mheshimiwa Jafo tunamshukuru alifika; je, Serikali sasa inasaidiaje pamoja na kuwa imetoa pesa kwa ajili ya kujenga hospitali za wilaya nyingine wakati bado hazijajengwa?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba ukienda Manispaa ya Iringa na kwa kuanzia hospitali ya mkoa ina wagonjwa wengi sana, ndiyo maana Serikali katika kuhakikisha kwamba tunapunguza mlundikano wa wananchi kwenda kutibiwa katika hospitali ya mkoa, ikawa ni wajibu kuhakikisha kwamba inajengwa hospitali ya wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama anavyotoa maelezo kwamba ile hospitali ya wilaya haijakamilika kwa kiwango ambacho kilitarajiwa, naomba nimhakikishie, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba hospitali zote za wilaya ambazo zinajengwa zinakuwa katika kiwango ambacho tunakitarajia ili mwananchi akipata rufaa kutoka kituo cha afya akienda kutibiwa kwenye hospitali ya wilaya apate matumaini kwamba nimefika katika hospitali ambayo hakika kwa majengo na huduma ataweza kupona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie, kwa kadri bajeti itakavyokuwa imeruhusu tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba suala la afya ni kipaumbele kama Serikali ilivyoelekeza.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali madogo ya nyongeza. Kwanza nianze kumshukuru Waziri kwa majibu yake, lakini naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa huu mradi ni muhimu sana na una tija sana katika manispaa yetu na ni mradi ambao kwa kweli toka mwaka 2008 umeanzishwa na ni chanzo kizuri sana cha mapato kama ambavyo amesema kwenye jibu lake. Pia tulikuwa tunategemea kwamba kama ungekamilika, ungeweza kutoa ajira zaidi ya 200 katika Manispaa na katika Mkoa mzima wa Iringa. Katika majibu yake, Serikali bado haijatoa commitment ya mradi huu kwa sababu tulikuwa tunategemea kwamba kama mradi huu ungekamilika kwa wakati…
Je, hiyo pesa ambayo inahitajika katika mradi huu Serikali inaji-commit vipi maana ni mradi ambao tunategemea kwamba utaweza kusaidia hata miradi mingine katika manispaa yetu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naomba kwanza nimpongeze Balozi wa Comoro, Mheshimiwa Mabumba kwa sababu aliweza kuwaalika wafugaji wanaotoka Tanzania kwenda kuona fursa zilizoko katika nchi ya Comoro na kwa kweli tuliona kuna soko kubwa sana la nyama, ng’ombe na la mbuzi. Je, Serikali sasa inawasaidiaje wafugaji kuunganishwa na masoko hayo katika nchi hiyo ya Comoro au nchi nyingine ili iweze kuleta tija katika nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza amezungumzia juu ya commitment ya Serikali katika kuhakikisha kwamba mradi huu wa machinjio ya Manispaa ya Iringa unaweza kupata pesa na hatimaye unakuwa ni chanzo cha mapato cha Halmashauri na kuzalisha ajira. Nimpongeze sana Mheshimiwa Ritta Kabati kwa kazi kubwa anayoifanya kwa ajili ya watu wa Iringa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama yeye mwenyewe Mheshimiwa Ritta Kabati unafuatilia vizuri ataona kwamba hivi sasa Serikali imekuwa ikifanya miradi ya kielelezo ya kusaidia Halmashauri zetu ziweze kujizalishia kipato chao wao wenyewe. Nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa aliyokwishaianza kwa ajili ya Maispaa za Mkoa wa Dar es Salaam na kwingineko katika Taifa letu. Zimetolewa pesa nyingi kwa ajili ya miradi ya kielelezo ikiwemo ya machinjio kama machinjio ya Vingunguti imepata pesa nyingi ili iweze kufanya vizuri na kuwa na tija. Nina imani kwamba baada ya kumaliza Dar es Salaam vilevile Serikali inaweza ikafanya kazi ya kuelekea katika maeneo mengine ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ameuliza juu ya namna sisi Wizara ya Mifugo na Uvuvi tulivyojipanga katika kuhakikisha wafugaji wetu wanapata masoko. Kama Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine watakuwa wafuatiliaji wazuri wataona kazi kubwa tunayoifanya. Katika kuhakikisha tunatangaza mifugo yetu na tunapata soko nje sisi katika Wizara tuna Idara inayoitwa Idara ya Huduma za Mifugo na Masoko na tunayo Bodi ya Nyama ambayo kazi yake ni kutafuta masoko nje ya nchi na kuitangaza nyama yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, tunatoa ushauri na kuangalia ubora wa nyama yetu ili iweze kupata masoko nje. Kusema ukweli hivi sasa tumekuwa tukipata masoko makubwa sana. Katika mwaka wa 2004 tulikuwa tunauza tani zisizozidi tatu, mwaka wa 2016/2017 tumeuza zaidi ya tani 1,000 za nyama nje ya nchi kutoka Tanzania. Mkakati wetu ni kuhakikisha tusiingize nyama ndani ya Taifa letu, badala yake sisi tuwe na uwezo wa kutoa nyama nje ya nchi. Kwa hiyo, tunaomba Waheshimiwa Wabunge, watuunge mkono kuhakikisha jambo hili kama Wizara tunaendelea nalo na tunaweza kufanikisha ajenda yetu ya Tanzania ya Viwanda hasa ile inayohusu mazao yetu ya nyama na samaki.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika Mkoa wetu wa Iringa kuna magari ambayo huwa yanaharibika tu kidogo yanawekwa katika vituo lakini tumekuta kuna mlundikano mkubwa sana wa magari mabovu. Ni kwa nini Serikali sasa aidha itengeneze au iyauze haraka sana ili yaweze kusaidia upungufu mkubwa ulipo katika Mkoa wetu wa Iringa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Ritta kwa wazo alilotoa. Niseme tu kama Serikali tunapokea ushauri huo, tutayatengeneza yale yanayotengenezeka na tutafanya utaratibu wa kuyauza yale yasiyoweza kutengenezeka.
Mheshimiwa Spika, kuhusu maoni yako upande wa pikipiki nilishatoa maelekezo kwamba vijana wa bodaboda wanaokamatwa kwa makosa madogo madogo wafanyanyiwe utaratibu wa kuandikisha na kuruhusiwa waendelee na kazi zao ili waweze kulipia kama kuna faini ambazo walitakiwa kulipa kuliko kuzirundika pikipiki hizo na zingine kuweza kuharibika wakati wangeweza kulipia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la mwisho, juzi sikukuona pale Uwanja wa Taifa, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kwenda pale kwa sababu kwa kweli kwa matokeo yale kama Rais asingekuwepo viti visingebaki salama. (Makofi/ Kicheko)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo ya nyongeza, lakini kabla sijauliza nilikuwa naomba nisahihishe jina langu, naitwa Ritta Enespher Kabati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri na mpango wao kabambe wa umwagiliaji, naomba nimwulize maswali mawili.
Kwa kuwa mradi huu wa Mkoga umekuwa ni mradi wa muda mrefu sana toka umeanzishwa katika Manispaa yetu. Tulikuwa tunategemea kama mradi huu ungekamilika, ungeweza kunufaisha zaidi ya wananchi 400 wakiwemo akina mama na vijana kuweza kujiajiri katika kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri anihakikishie katika mwaka wa fedha 2019/2020 kama Serikali itaweza kutoa pesa ili kuweza kuukamilisha huu mradi ambao umekuwa wa muda mrefu sana? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, nilikuwa nataka kuuliza kwamba kwa kuwa katika Manispaa yetu hii ya Iringa bado tunao mradi mwingine wa Kitwiri Irrigation mradi ambao pia toka umeanzishwa haujawahi kupatiwa fedha, je, ni lini utapatiwa fedha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile namwomba Mheshimiwa Waziri kama yuko tayari kuja sasa katika mkoa wetu wa Iringa ili aitembelee hii miradi yote miwili na vilevile atembelee hata miradi mingine ya mkoa wetu wa Iringa ili iweze kukamilika na iweze kunufaisha wananchi wa mkoa wetu wa Iringa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, mama yangu Mheshimiwa Ritta Kabati, ni mmoja ya wamama shupavu sana katika kuhakikisha wanatetea matatizo ya wananchi wao katika Mkoa wa Iringa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati ya moyo wangu, tumekuwa na miradi mingi sana katika umwagiliaji zaidi ya 2000 lakini ni miradi 960 tu ndiyo iliyoendelezwa, zaidi ya miradi 1,967 haijaendelezwa. Sisi kama Wizara ya Maji, tukitambua kabisa umwagiliaji ndiyo kilimo mbadala ambao kinaweza kuchangia uchumi wa nchi yetu, tumeona haja sasa ya kuunda Tume ambayo itapitia mpango kabambe wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ili tuwe na miradi michache ambayo itakuwa na tija kubwa sana katika nchi yetu kwa sababu tumekuwa na miradi mingine haina hata chanzo cha maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia suala la umwagiliaji, maana yake ni kilimo cha mbadala. Tunajua kabisa nchi yetu wakulima wengi wanalima kwa kutegemea kudra za Mwenyezi Mungu mpaka mvua inyeshe. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie, katika mpango huu kabambe tutakaoupitia katika mradi huu wa Mkoga, tutaupa kipaumbele katika kuhakikisha tunaukamilisha ili wananchi wake wa Iringa waweze kunufaika na kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili kuhusu mimi kwenda Iringa, nataka nimwambie mwenda kwao haogopi kiza. Nitakwenda Iringa katika kuhakikisha naenda kuzungumza na wananchi wa Iringa ahsante sana. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali ya nyongeza. Kwanza kabisa nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri ambayo amenipatia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa Serikali imefungua mradi wa REGROW ambao utafanya kazi ya kukuza utalii wa ukanda wa Kusini ukiwemo Mkoa wa Iringa; je, Serikali ina mkakati gani wa kujengea uwezo wananchi waliopo katika mkoa wetu ili watumie vizuri fursa hiyo kujiajiri na kuweza kujipatia kipato? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa nje ya maeneo ya utalii kuna historia kubwa za machifu akiwemo Mtwa Mkwawa, lakini kuna Kituo cha Kalenga, eneo la Mlambati ambapo Mwalimu Nyerere aliweka jiwe la msingi mwaka 1998 kama ukumbusho wa miaka mia moja.
Je, ni lini Serikali itachukua ya kuyaboresha kwa ajili ya kuvutia watalii na kuhakikisha kwamba pesa inayopatikana katika maeneo hayo, inawasaidia wananchi wanaozunguka eneo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kabla sijajibu haya maswali nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza kwa jinsi ambavyo amesimama imara katika kuupigania Mkoa wa Iringa, lakini pia alipigania sana kuhakikisha kwamba Kituo cha Utalii kinajengwa pale Kihesa, Kilolo. Kwa kweli nampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maswali yake ameuliza; je, tuna utaratibu gani wa kuhakikisha tunawajengea uwezo? Naomba nichukue nafasi hii kusema kwamba katika mradi mkubwa ambao tunaenda kuutekeleza Mikoa ya Kusini unaohusu hifadhi nne yaani Udzungwa, Mikumi, Ruaha pamoja na Selous ya Kaskazini, tuna utaratibu wa kuimarisha miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili wananchi wa Mkoa wa Iringa waweze kufaidika na huu mradi, ni lazima wajengewe uwezo ili waelewe umuhimu wa kuuendeleza utalii na wawe tayari kuwakarimu watalii watakaokuwa wanatembelea katika Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hivi sasa tuna mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba, kwanza tunawaelimisha namna ya kuanzisha makampuni ya kitalii ya kuongoza watalii, lakini pili, namna watakavyowakarimu pamoja na kuwaonyesha mambo mbalimbali ambayo yapo katika Mkoa wa Iringa ukiwemo utamaduni wa Iringa na tatu, ni pamoja na kuwapokea na kuwakarimu katika hoteli mbalimbali. Kwa hiyo, hii mipango yote tutaitekeleza katika mwaka wa fedha huu unaoanza Julai. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu kile Kituo cha Kalenga, kama alivyosema kweli kabisa miundombinu bado haitoshelezi. Hivi sasa tuna mpango kabambe wa kuhakikisha barabara ya lami inajengwa kutoka Iringa hadi kwenye lango kuu la Ruaha. Wakati tutakapokuwa tunajenga ile barabara, tutaangalia uwezekano wa kuimarisha ile miundombinu, kuchepusha pale kupeleka katika hiki Kituo cha Kalenga kwa sababu ni karibu ili tuhakikishe kwamba nako panafikika kiurahisi. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa swali dogo la nyongeza. Nimpongeze kwanza Mheshimiwa Waziri wa Maji kwa kuja katika Mkoa wetu wa Iringa na kujionea jinsi ambavyo Mji wetu wa Iringa ulivyokua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kuuliza swali dogo; kwa kuwa Mji wa Iringa unakua kwa kasi kubwa sana, kuna baadhi ya maeneo ambayo hayapati maji kama kule Tagamenda, Isakalilo na Kigonzile. Je, Serikali ina mpango gani wa kutuletea pesa ili kuongeza ule mtambo wa kusambaza maji pamoja na kuwa sasa hivi tunapata asilimia 96, lakini maji yetu tunaweza tukapata asilimia 100?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Chama cha Mapinduzi wakati inajenga mtambo wa kutibu maji Iringa iliweka matoleo ili population itakapoongezeka basi tuweze kupanua ili maji yaweze kuongezeka. Katika mwaka ujao wa fedha tumetenga bajeti kwa ajili ya kuanza kupanua mtambo wa kutibu maji ili maji yaweze kuenea katika kata zote.
MHE. RITA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi, ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa katika Manispaa yetu ya Iringa kuna Daraja la Igumbiro, daraja ambalo limekuwa likileta maafa kila mwaka na ambalo limechukua muda mrefu sana kumalizika. Je, ni lini sasa Serikali itatoa pesa ili Daraja lile la Tagamenda liweze kukamilika?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo ambayo tunafanya uwekezaji mkubwa wa miundombinu ni pamoja na Manispaa ya Iringa. Serikali ya Chama cha Mapinduzi imeamua kuboresha miundombinu katika Manispaa hiyo ya Iringa na hivi sasa tumekamilisha barabara kadhaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Ritta Kabati kwamba wataalam wangu wataenda kufanya tathmini katika eneo hilo ambalo limebakia linaonekana lina changamoto. Lengo letu kubwa ni ili tuhakikishe kama hiyo kazi ina upungufu wa aina yoyote tuweze kuurekebisha ili wananchi wa Iringa wawe katika mazingira mazuri ya kuweza kusafiri.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.
Kwanza kabisa naomba nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri alipokuwa anakwenda Mbeya alipitia katika hospitali yetu ya Iringa na akajionea changamoto kubwa kabisa ambazo ziko katika mkoa wetu. Kwanza kabisa ni udogo wa eneo la hospitali ambayo iko katika mkoa wetu ambayo kwa kweli pia kuna muingiliano wa Magereza. Tatizo kubwa Madaktari Bingwa hawana kabisa maeneo ya kuishi kwenye lile eneo na wagonjwa wanapata shida sana wanapokuja kutibiwa usiku na vilevile alielezwa kuhusiana na eneo ambalo mkoa umeutafuta ili kuwepo na alternative mbili aidha magereza itoke au walipie lile eneo ili madaktari wetu waweze kuwasaidia wagonjwa usiku.
Je, sasa Serikali inatuambiaje maana yake hili ni tatizo la muda mrefu ili wananchi wa Mkoa wa Iringa waweze kutatua hiyo changamoto? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Ritta Kabati kwa sababu jambo hili amekuwa akilifuatilia sana na hii inaonyesha ni jinsi gani anavyojali masuala ya ustawi wa wananchi wa Iringa Mjini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani imelitafakari sana jambo hili na kuona kwamba kilicho rahisi kuhama ni Magereza kwa sababu kwanza eneo lipo na lipo ndani ya Manispaa na kiusalama liko vizuri zaidi kuliko pale ambapo wagonjwa au ndugu wanaoenda kuwaona wagonjwa hulazimika kupita mbele ya geti kubwa la gereza ambacho kiulinzi inaleta matatizo. Kwa maana hiyo sisi kama Wizara tunaendelea tu kuangalia logistic za kibajeti ili tuweze kuanza utaratibu huo wa kuhamisha gereza ili kutoa fursa nzuri ya wananchi kuweza kupata matibabu na expansion ya Hospitali ya Mkoa kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kumekuwa na ongezeko kubwa sana la vijana wetu kutumia madawa ya kulevya na kwa kuwa sober nyingi sana zinamilikiwa na watu binafsi na kwa kweli zimekuwa zikifanya vizuri, lakini gharama za kuziendesha tunaona ni kubwa kiasi kwamba vijana wengi wanashindwa kumudu gharama zake. Je, ni kwa nini sasa Serikali isitoe ruzuku kwa hizi sober house za watu binafsi au kuanzisha za kwake ili kusaidia vijana wetu kurudi katika hali zao?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakiri kwamba kumekuwa na tatizo la dawa ya kulevya na Serikali imechukua juhudi
na hatua ya kuhakikisha kwamba tunadhibiti uingizaji wa dawa za kulevya na kwa kiasi kikubwa kwamba tumepunguza sana matumizi ya madawa za kulevya hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tunatambua vilevile kwamba kuna wahanga ambao walikuwa wanatumia hizi dawa za kulevya, sisi Serikali tumeendelea tukishirikiana na wadau binafsi. Kwa upande wa Serikali tumeanzisha vituo mbalimbali vya matibabu katika hospitali zetu za Mkoa wa Dar es Salaam, Mwanza, Mbeya na hivi karibuni tumezindua hapa Itega Dodoma, lakini tunatambua mchango mkubwa wa sober houses na sisi kama Serikali tumetoa mwongozo wa usimamizi wa hizi sober houses, lakini sasa hivi bado ni mapema sana kusema kwamba Serikali itakuwa inachangia Ruzuku kwa uendeshaji wa hizi sober houses.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba niulize maswali madogo tu mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, naomba niipongeze Serikali kwa majibu yake mazuri, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa tamko lake ambalo limehakikisha kwamba wazabuni wote wanalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna baadhi ya wazabuni wakiwemo hata wa Mkoa wangu wa Iringa wameshafanyiwa uhakiki zaidi ya mara moja, lakini wanadaiwa na mabenki, wanadaiwa na TRA na wanatishiwa mpaka kuuziwa mali zao:-

Je, Serikali inawasaidiaje wasifilisiwe? Maana wengi wao tayari wameshapata maradhi na kufa na wengine wameshafilisika kabisa kwa ajili ya madeni ambayo wanaidai Serikali.

Swali langu la pili; je, ni vigezo gani sasa vinatumika kwenye malipo ya madeni ya wazabuni hao?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la kwanza kuhusu msaada wa Serikali ili wananchi wetu wasifilisiwe, naomba kumwambia Mheshimiwa Rita na kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, tunalipa madai pale yanapokuwa yamehakikiwa. Wananchi wetu hawa wa Mkoa wa Iringa, kama wapo ambao madeni yao yamehakikiwa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Ndani wa Serikali, basi tumekuwa tukiwasaidia mmoja baada ya mwingine wanapofika na kuwasilisha nyaraka zao kuonyesha kwamba wamehakikiwa na sisi kujiridhisha kwamba wapo kwenye orodha ya kulipwa ndani ya Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Ritta na nimpongeze kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya katika kuwatetea wananchi wa Iringa. Ameshakuja siyo mara moja wala mara mbili ofisini kwangu, naomba tuendelee kushirikiana ili tuwasaidie wananchi wetu ili wasifilisiwe na ili wasiendelee kupata maradhi kama wapo kweli waliopata maradhi. Tuendelee kushirikiana tuwasaidie wananchi hawa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, ameuliza ni vigezo gani vinavyotumika kulipa madai haya ya wazabuni pamoja na wakandarasi wengine? Kwanza kabisa ni kuhakikisha deni limehakikiwa na limekidhi vigezo vya kuwa deni halali. Hicho ni kigezo cha kwanza kwamba deni hilo linalipwa.

Mheshimiwa Spika, sababu ya pili au kigezo cha pili ambacho kinapelekea kulipwa, tunaangalia deni lile kama hali-attract riba kwa Serikali, lakini pia kwa yule ambaye anaidai Serikali. Kama deni hili lina-attract riba tunayapa kipaumbele ili Serikali isiendelee kuumia na ili tusiendelee kuwaumiza wananchi wetu ambao wanaidai Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, kigezo cha tatu ni kuhakikisha kwamba ukubwa wa deni lenyewe, kwa wale ambao wana madeni ambayo siyo makubwa na ambao ndio wengi tumekuwa tukiwapa kipaumbele kuhakikisha kwamba tunawalipa madeni yao kwanza ili kuweza kuchachua uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana mwaka 2017/2018 Bunge lako Tukufu lilitupitishia bajeti ya shilingi trilioni moja kwa ajili ya kulipa madeni haya na Serikali ililipa zaidi ya shilingi trilioni 1.096 kwa sababu dhamira ya Serikali yetu ni njema kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Spika, kigezo cha nne, ni umri wa deni. Madeni yale ambayo yamekaa kwa muda mrefu na tayari yamehakikiwa, tumekuwa tukiyapa kipaumbele na kuhakikisha yote yanalipwa ili kuwawezesha wananchi wetu kuendelea kushiriki katika shughuli za kiuchumi.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Magufuli kwa uzinduzi wa barabara ya kutoka Makambako mpaka Mufindi jana. Naomba niulize swali moja. Katika ujenzi wa barabara ya kutoka Dodoma - Mtera mpaka Iringa, pale katika kona za Nyang’holo huwa kunakuwa na maporomoko makubwa sana ambayo huwa yanajitokeza hasa wakati wa mvua:-

Je, Serikali inatusaidiaje? Maana kutakuja kutokea ajali kubwa sana, hata jana nimepita pale. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tayari ameshafika ofisini zaidi ya mara tatu akifuatilia kipande cha barabara hii ya kutoka Mtera - Iringa hasa kwenye kona zile za Nyang’holo ambazo ni korofi kabisa. Tunakiri na bahati nzuri nimeshamwelekeza Meneja wa TANROAD Mkoa kufuatilia eneo hilo ili tuanze tararibu za kulirekebisha kwa ajili ya usalama wa Watanzania.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali moja la nyongeza. Kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa Muungano umetuletea faida nyingi sana katika nchi yetu na ndiyo maana viongozi wetu, waasisi na sisi wenyewe tumekuwa tukiuenzi na kuulinda kwa nguvu zote na kwa kuwa sasa huko vijijini vijana wetu wengi wamekuwa hawana uwelewa sana wa kutosha kuhusiana na huu Muungano. Je, ni ni kwa nini sasa Serikali isiweke utaratibu wakati wa sherehe hizi elimu itolewe kwa ajili ya vijana wetu na wananchi walioko vijijini kuliko kufanya sherehe kitaifa zaidi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati kwa niaba yake ambapo swali la msingi lilikuwa la Mheshimiwa Martha Moses Mlata. Kwanza kabisa nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mlata kwa swali hili ambalo litatoa ufahamu mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kutoa rai, siku ya tarehe 26 nafahamu itakuwa siku ya Ijumaa mwezi wa Nne kwamba Taasisi zote za Elimu zitumie fursa hii ya kutoa elimu kuhakikisha kwamba wanakuwa na makongamano na mijadala mbalimbali juu ya historia ya Muungano wetu. Ahsante.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kukubaliana kwamba kuna unyanyasaji mkubwa sana kwa wanawake na watoto lakini upo unyanyasaji mkubwa sana kwa kina baba, wapo ambao wamekuwa wakipigwa na wengine kunyanyasika. Kuna maandamano ambayo tuliona katika mitandao katika nchi ya jirani ya Kenya akina baba wakiandamana kudai haki zao za msingi kwa akina mama. Je, ni lini sasa sheria pia itajengwa kuwalinda akina baba ambao wamekuwa wakinyanyasika kila wakati?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge Viti Maalum, Mkoa wa Iringa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inapoongelea ukatili wa kijinsia haimaanishi tunaongelea ukatili wa akina mama na watoto, jinsia ina cut-across na akina baba. Bahati mbaya sana matukio ya ukatili wa kijinsia ya akina baba siyo mengi yanakuwa reported. Nitumie fursa hii kuwaomba wale akina baba ambao nao wanapigwa, wanafanyiwa ukatili wa kingono, wanaonyanyaswa kisaikolojia nao waweze kujitokeza ili madawati yetu ya jinsia yaweze kuyafanyia kazi.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kumekuwa na tatizo kubwa wananchi kubambikizwa kesi hasa kwenye hizi kamera, mtu unapigwa kamera ukienda kuhoji wanasema kwamba imekosewa namba ya gari kwa hiyo wananchi wengi wamekuwa wanabambikiziwa makosa ambayo si ya kwao. Je, Serikali inasemaje kuhusiana na kamera ambazo zimekuwa zinawabambikia wananchi makosa ambayo siyo ya kwao.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi haya ya teknolojia tumeanzia na kamera, tuna mfumo VTS na tuna mambo mengine mengi ambayo tunaelekea nayo huko, yote haya yana dhamira ya kupunguza hizo dhana dhidi ya askari wetu kuhusiana na kubambikia watu makosa.

Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba matumizi ya tochi yamekuwa yakitusaidia sana. Hata hivyo, ikiwa kuna changamoto upungufu wa kimaadili wa baadhi ya askari wetu na hilo hatuwezi kulikataa kwa sababu askari nao ni binadamu huwezi kuwa na askari wote hawa wakose wawili watatu ambao watakuwa na upungufu wa kimaadili, tumekuwa tukiendelea kuchukua hatua pale ambapo tunapata taarifa na uthibitisho juu ya kubambikia wananchi makosa ambao hawahusiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumsisitiza Mheshimiwa Mbunge kwamba tusaidiane kwa pamoja kufichua wale askari wachache ambao watakuwa wanatuhumiwa ama wanajihusisha na tabia kama hizo zilizokuwa kinyume na maadili ya utendaji kazi wa Jeshi la Polisi.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa utekelezaji wa miradi ya maji unategemea na mpango wa fedha, natambua kuna baadhi ya Wakandarasi bado hawajalipwa fedha zao: Je, ni lini sasa Mkandarasi ambaye anatekeleza mradi wa Mji Mdogo wa Ilula katika Jimbo la Kilolo atapatiwa malipo yake ili wananchi wa Ilula waache kupatiwa migao ya maji mara kwa mara?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuwapigania akina mama na Watanzania hususan katika suala zima la maji. Kikubwa, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Kama unavyoona, gari haliwezi kwenda bila mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tulikuwa tunadaiwa takribani zaidi ya shilingi bilioni 88 na Wakandarasi, lakini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Wizara ya Fedha, wametupatia fedha zote shilingi bilioni 88 ambazo tulikuwa tunadaiwa na Wakandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, katika mradi wake ule wa Ilula kwa Mheshimiwa Mwamoto, Kilolo pale, tumeshamlipa zaidi ya shilingi bilioni moja. Tunataka zile fedha tulizomlipa sasa awekeze pale katika kuhakikisha anakamilisha mradi na wananchi wa Ilula waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatolesheleza.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza niipongeze Serikali kwa kuweka mpango mzuri kabisa wa elimu kwa watoto wetu kwamba watoto wote wanahakikisha wanapata elimu, lakini bado kuna wazazi ambao kwa mfano pale Dar es Salaam wanakaa pale barabarani wanawatuma watoto kwenda kuomba kwenye magari, sasa wale watoto wanakosa haki kabisa ya msingi ya kusoma.

Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba watoto wetu wale wanasoma na wale wazazi wanachukuliwa hatua?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza katika majibu yangu ya nyongeza kwa Mheshimiwa Chikambo, watoto, labda kwa faida ya Bunge lako tukufu, Tanzania tumeridhia Mkataba wa Kimataifa na sisi tukaanzisha Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 ambayo inatoa haki kwa watoto. Mtoto ana haki ya kutunzwa, mtoto ana haki ya kuendelezwa, mtoto ana haki ya kushirikishwa katika maamuzi yanayomhusu na mtoto ana haki ya kutokutumikishwa kazi nzito.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ukiangalia katika sheria hii utaona hapa tunagusa katika maeneo makubwa mawili; kwanza haki ya mtoto ya kuendelezwa, lakini haki ya mtoto kutotumikishwa kazi nzito. Serikali tumeendelea kuchukua hatua mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, lakini naomba nitumie fursa hii sasa kuongea na kuziagiza Halmashauri za manispaa na majii kuhakikisha kwamba, wanasimamia kikamilifu sheria hii ya mtoto na ili watoto wale waweze kupata haki yao ya msingi ya kuendelezwa kwa maana ya kusoma, lakini pili kutokutumikishwa kazi na badala yake wale watoto waweze kukaa shuleni na kupata elimu. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa changamoto iliyopo katika Bypass ya Babati inafanana kabisa na katika Jimbo letu la Iringa Mjini ambako Serikali imeshabomoa makazi ya watu lakini ujenzi haujaanza. Je, Serikali itaanza lini ujenzi huo ili kupunguza adha kubwa kabisa wanayopata wananchi kwenda katika stendi mpya ya Igumbilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejipanga kuijenga barabara hiyo ni kilomita Saba na katika bajeti ya mwaka huu tumetenga fedha kuanza ujenzi wa barabara hiyo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ritta Kabati ninakupongeza tu unafuatilia sana barabara hii lakini nikuhakikishie pia kwamba tumejipanga vizuri tunajua usumbufu wananchi wa Iringa Mjini wanaopata wa magari makubwa yanayopita katika ya Mji, kwa hiyo ujenzi wa barabara hii utaanza tu mara moja kwa sababu tumeshajipanga vizuri na tutaendelea kutoa feedback. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza:

Kwa kuwa watoto wengi sana wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya kikatili na wamekuwa wakiathirika kisaikolojia. Ni kwa nini Serikali sasa isiwe na mpango maalum wa kuanzisha haya madawati katika shule, kwa sababu watoto wanavyofanyiwa vitendo vya kikatili wanashindwa kwenda katika madawati huko mtaani? (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Ritta Kabati kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya katika masuala ya kupambana na vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto ikiwemo kwa wananchi wa Iringa, ninaamini wanawake wa Iringa watamrudisha Bungeni ili aendelee kuwasemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tumeona kwamba watoto wengi wako katika shule zetu, shule za msingi na shule za sekondari, kwa hiyo kama Wizara tayari tumemuandikia Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Jafo ili sasa tumemuelekeza kwamba katika kila shule ya msingi na sekondari ya Serikali na shule Binafsi kuanzishwe madawati ya ulinzi na usalama wa watoto katika maeneo ya shule ili pale mtoto ambapo amefanyiwa vitendo vya ukatili kwa sababu pia wazazi hatuna muda majumbani, kwa hiyo, angalau pale akiwepo katika mazingira ya shule mtoto ataweza kujua kwamba anaenda katika sehemu gani na ni Mwalimu gani na katika muda gani naweza kueleza matatizo yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumewaelekeza Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Kata zote wawe pia wanatembelea shule hizi na Maafisa Ustawi wa Jamii mara kwa mara kwa ajili ya kutoa elimu lakini kuwasikiliza watoto ambao wanafanyiwa vitendo hivi vya ukatili. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ritta ninaahidi tu kwamba tayari tumeanza kufanyia kazi na tunaendelea na majadiliano na wadau wetu ili angalau tuanze katika Mikoa ambayo vitendo vya ukatili dhidi ya watoto ni vingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua na wewe masuala haya huwa yanakugusa kwa karibu zaidi. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Vijiji wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana katika maeneo yetu lakini wengi wao hawana ofisi na wengineo wanatumia nyumba zao kama ofisi:-

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba Wenyeviti wetu wanapata ofisi ili waweze kufanya kazi zao vizuri sana katika Halmashauri zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, nashukuru. Ni kweli kuna baadhi ya maeneo ambayo Wenyeviti wetu wa Vijiji na Mitaa hawana ofisi, lakini wengine wamepanga katika nyumba za watu binafsi na wakati mwingine wanalazimika kufanya kazi hizo za kuhudumia wananchi katika majengo yao binafsi. Maelekezo ya Serikali ni kwamba Wenyeviti wa Mitaa ofisi zao zinasimamiwa na Halmashauri na Wakurugenzi katika maeneo yao, kwa sababu Watendaji wa Mitaa na Vijiji ni Wawakilishi na wanafanya kazi kwa niaba ya Mkurugenzi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nielekeze Halmashauri zote, kwenye bajeti zao za kila mwaka lazima watenge bajeti ya kujenga ofisi hata kama siyo zote, ndiyo maelekezo. Nasi tunaendelea kufuatilia na tuna taarifa za Halmashauri kuna baadhi wameanza kujenga ofisi hizo kwa kupitia michango mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge pia, nimeona kwenye taarifa kwamba kwenye Mfuko wa Jimbo baadhi ya Wabunge tena wengine wa Viti Maalum wamechangia ujenzi wa Ofisi za Mitaa na Vijiji, lakini kuweka zana kama photocopy machine na kusaidia utendaji uweze kuboreshwa.

Mheshimiwa Spika, tuwahimize Wakurugenzi kile kinachopatikana kila mwaka kwenye bajeti yao na Waheshimiwa Wabunge wafuatilie, tutenge kiasi kidogo ili kuweza kupunguza shida za Ofisi za Wenyeviti wetu wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji. Ahsante.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa watu wenye ulemavu wamekuwa wakipata shida sana wanapokwenda kutibiwa katika hospitali zetu kwani kumekuwa hakuna mawasiliano kati ya daktari na mtu mwenye ulemavu kwa sababu ya daktari kutojua lugha za watu wenye ulemavu. Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba wanaweka mkalimani kati ya daktari na mtu mwenye ulemavu ili aweze kutibiwa kile ambacho anatakiwa kutibiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WATU WENYE ULEMAVU (MHE. STELLA IKUPA ALEX): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala ambalo ameliuliza Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi kwamba tuna upungufu wa wakalimani wa lugha ya alama. Wizara ya Afya ilishatoa maelekezo kwamba kwa kuwa sasa hivi tunajiandaa na tunawaandaa wakalimani wa lugha za alama basi watu wenye ulemavu wanapoenda hospitali waruhusiwe kwenda na watu ambao wanawaamini ili mawasiliano yaweze kufanyika vizuri kati ya mtu mwenye ulemavu na daktari ama na mtu anayemhudumia.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la maji. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofanya ziara katika mkoa wetu wa Iringa aliweka jiwe la msingi katika mradi mkubwa sana wa maji katika Mji Mdogo wa Ilula:-

Je, ni lini sasa mradi ule utaanza kufanya kazi ili wananchi wa Iringa waweze kutuliwa ndoo kichwani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, anatosha sana mama yangu kwa kuwapigania…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri!

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa ambacho nataka kusema, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha, mkandarasi ame-raise certificate kwa ajili ya kumlipa. Tutamlipa kwa wakati.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo mawili. Kwanza nianze na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri sana ambazo wamekuwa wakizifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze sana Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi kwa ujenzi wa mtandao wa barabara katika Mkoa wetu wa Iringa, wamefanya kazi nzuri sana. Pia kuwalipa wananchi hao fidia kwa hiyo barabara ambayo imetajwa hapo.

Katika majibu yake Mheshimiwa Waziri amekiri kwamba wananchi hao wanatakiwa walipwe fidia na riba, sasa nimuombe Waziri anijulishe. Je, ni lini? Na wanalipwa bila usumbufu kwa sababu kwa kweli kwanza walitumia karibu miaka mitano kutolipwa baada ya tathmini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa changamoto ya kupitisha magari makubwa katikati ya Mji wa Iringa kumesababisha wafanyabiashara hasa wenye maduka, hoteli, migahawa kupata shida sana na wale wananchi wanaofuata huduma kwa sababu magari yao yanafungwa, kwa hiyo wanasababisha kutofanya biashara vizuri. Vilevile kumesababisha Serikali kutopata kodi ya uhakika na vilevile kuna ajali kubwa sana itakuja kutokea kwa sababu magari makubwa ya mafuta yanapita barabarani.

Je, Mheshimiwa Waziri sasa leo hii uniambie na uwaambie wananchi wa Iringa ile barabara ya mchepuo kwa sababu tumeshapata ahadi nyingi sana. Kila siku, nimeuliza kama maswali matano, lini sasa mtaijenga ili kuondoa hiyo changamoto ambayo imekuwa ni tatizo kubwa mno katika Mkoa wa Iringa? (Makofi)
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mbunge Viti Maalum, Mheshimiwa Ritta Kabati kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza suala la riba ni commitment ya Serikali kwamba riba hiyo kwa wananchi italipwa baada ya fedha kutolewa kwa sababu tuko mwezi wa tisa na kwa mujibu wa sheria za kifedha, mwezi wa tisa ndiyo fedha zinaanza kutolewa. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Ritta Kabati kwamba fedha hiyo ya riba italipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu usumbufu mwingine uliousema Serikali ilishaona, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwamba kuna umuhimu wa kuweka barabara ya mchepuo ili kuweza kuondoa hivyo vikwazo ambavyo mwenyewe umevitaja kwa wananchi. Kwa hiyo, nikuhakikishie, usanifu umekamilika na kama hatua tayari fidia tumeshalipa bado riba. Kwa hiyo sasa hivi taratibu za Kiserikali zinaendelea ili kuhakikisha barabara hiyo inajengwa haraka. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize maswali ya nyongeza na nishukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa umbali yalipo mahabusu, Ofisi ya OCD, karibu kilometa 70 mpaka yalipo Makao Makuu ya Kilolo, hivi Serikali inatumia gharama kubwa sana kusafirisha mahabusu, kumsafirisha OCD na askari kwenda yalipo Makao Makuu. Je, Serikali huwa inaangalia tathmini ya gharama inazozitumia kwa kuchelewesha kujenga hizi Ofisi za Wilaya.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa nyumba za polisi zilizopo wilaya ya Mufindi, zilizopo FFU Kihesa na Central line polisi Iringa Mjini ni nyumba ambazo kwakweli ni chakavu mno, vyo haviingiliki, askari wetu wamekuwa wakiishi familia 5 chumba kimoja na kuna adha nyingi sana ambazo wanazipata hata watoto na kinamama ambao wanaishi katika zile nyumba.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri anipe siku, tarehe na mwezi ambao tutakwenda kukagua nyumba zote za Mkoa wa Iringa na kubwa ambazo wamekuwa wakizipata askari wetu walioko katika Mkoa Iringa, ili mwenyewe ajionee na aone jinsi gani ambavyo pamoja na ufinyu wa bajeti yeye mwenyewe ataona kwamba iko haja sasa haya majengo ya Askari au nyumba za askari ziweze kukarabatiwa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza kwa dhati ya moyo wangu Mheshimiwa Ritta Kabati, kwa jinsi ambavyo amekuwa akitetea sana Jeshi letu la Polisi katika Mkoa wa Iringi, lakini siyo kwamba amekuwa akitetea kwa maneno, ni miongoni mwa Wabunge ambao wameshiriki kikamilifu katika kuhakikisha kwamba wanapunguza changamoto za Askari wetu kwa yeye mwenyewe kujitolea kujenga kituo cha polisi kilichopo eneo la Semsema.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, baada ya pongezi hizi, Mheshimiwa Rita Kabati na jitihada kubwa ambazo tunaziona anazozifanya katika kupigania polisi, nimhakikishie kwamba tutaambatana mimi na yeye kwa ruhusu ya Mheshimwa Spika, ili twende tukashirikiane kwa pamoja kubabiliana na changamoto ambazo amezizungumza. Hata hivyo, nataka nimhakikishie kwamba tayari Serikali imeshaanza jitihada. Kwa mfano hivi tunavyozungumza kuna ujenzi wa nyumba sita unaendelea kwenye Makao Makuu ya FFU pale Iringa ni kuonesha kuguswa na upungufu na uchakavu wa nyumba za Askari katika Mkoa wa Iringa.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tayari kuna eneo ambalo tumelibaini kwa ajili ya ujenzi wa kituo kwa baadaye kwenye wilaya yake, tukitambua kwamba kuna umuhimu wa Makao Makuu ya Polisi ya Wilaya kuwa katika Makao Makuu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nadhani nimeshamjibu maswali yake mawili ya nyongeza kwa pamoja.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali ya nyongeza. Kwa kuwa Mkoa wetu wa Iringa ni mkoa ambao kwa kweli una baridi sana na wanafunzi wengi wamekuwa wakisoma kwa shida kutokan ana uchakavu mkubwa uliopo wa shule zetu za msingi. Na shule zetu nyingi za msingi toka zimejengwa hazijawahi kukarabatiwa, nishukuru baadhi ya wazazi wa Mkoa wa Iringa wamekuwa wakisaidia katika ukarabati na Mheshimiwa Waziri nafikiri alikuja akaona baadhi ya shule ambazo tumeanza kuzikarabati.

Je, Serikali iko tayari sasa kusaidia angalau kidogo baadhi ya shule ule ukarabati ambao wazazi wanafanya na Serikali ikasaidia japo kidogo ili tuweze kukarabati shule nyingi za Iringa?

Mheshimiwa Spika, swali letu la pili, kwa kuwa pia sambamba na hilo, shule nyingi za sekondari maabara nyingi hazijakamilika na wanafunzi wengi sana wamekuwa wakifanya mitihani bila kusoma vizuri kwa sababu ya kutomalizika kwa maabara.

Je, Serikali sasa inasemaje kuhusiana na kumalizia maabara ambazo bado hazijaisha ili wanafunzi wetu wa Iringa waweze kusoma na kufaulu vizuri?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya dada yangu, Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Mkoa wa Iringa pamoja na mikoa mingine ina changamoto hizo za uchakavu wa miundombinu. Lakini naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa sababu safari zangu za Mkoani Iringa tulivyofika pale katika Manispaa ya Iringa alienda kunionesha akiwa na timu yake pale, miongoni mwa shule ambazo yeye mwenyewe na wadau wenzake waliweza kushiriki katika ukarabati.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, lengo la Serikali yetu ni kuhakikisha tunafanya kila liwezekanalo kufanya ukarabati wa shule hizi ndiyo maana juzijuzi Serikali yetu imetoa zaidi ya shilingi bilioni 35.5 kwa lengo la kuhakikisha kwamba tunaongeza nguvukazi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kubadilisha miundombinu hiyo.

Mheshimiwa Spika, lakini hata hivyo, nikiri wazi kwamba katika suala zima la maabara kweli kuna changamoo kubwa, kama lengo la Serikali lilivyo kwamba agenda yetu kwa mfano katika bajeti ya mwaka 2019/2020 ambayo nimeiwasilisha hapa Bungeni siku chache zilizopita, zaidi ya shilingi bilioni 90.08 tunazielekeza katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, lakini karibuni bilioni 58 kati ya hizo zinaenda katika elimu ya sekondari na lengo letu kubwa ni kuhakikisha kwamba maabara tunaziimarisha katika maeneo yetu na ndiyo maana juzijuzi tumetoa fedha zaidi ya shilingi bilioni 16 ambazo tunakwenda kununua vifaa vya maabara kwa vijana wanapokuwa sekondari waweze kusoma vizuri masomo yao.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake lakini pia niendelee kumshukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Iringa, Dkt. Mwakalebela kwa kazi nzuri sana ambayo amekuwa akiifanya katika hospitali yetu kutokana na changamoto nyingi zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, Mkoa wetu wa Iringa unakabiliwa na ajali nyingi sana lakini kipindi kirefu hatuna daktari bingwa wa mifupa pia hatujawahi kupatiwa daktari bingwa wa watoto toka hospitali ile imeanzishwa. Tuna wodi kubwa sana katika hospitali yetu ya Mkoa kuliko hospitali zote za Nyanda za Juu Kusini.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri sasa anatupa ahadi gani wananchi wa Mkoa wa Iringa kutokana na changamoto hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, naomba niipongeze Serikali yetu hii ya Awamu ya Tano kwa ujenzi wa Hospitali za Wilaya katika nchi yetu. Mkoa wetu una upungufu mkubwa sana wa watumishi takriban asilimia 70 inawafanya wauguzi na madaktari kufanya kazi kwenye mazingira magumu sana. Je, nini mpango wa Serikali katika kukabiliana na changamoto hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Ritta Kabati amekuwa anafanya kazi nzuri sana ya kufuatilia masuala mbalimbali ya afya katika Mkoa wa Iringa. Kwa kweli amekuwa anatufuatilia sana sisi ndani ya Wizara na tunashukuru kuona kwamba ni mdau mkubwa sana katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza linahusiana na kwamba kuna upungufu wa madaktari wa upasuaji wa mifupa pamoja na madaktari wa watoto. Hilo kama Serikali nakiri lakini sasa hivi Serikali inafanya mkakati wa kufanya mafunzo ya madaktari bingwa takribani 100 mwaka jana tumesomesha, mwaka huu tunasomesha madaktari wengine zaidi ya 100. Wwale watakaomaliza mafunzo na tumeweka utaratibu kwamba madaktari bingwa ambao wanasomeshwa kwa fedha za Serikali baada ya kuhitimu masomo yao, sisi Serikali tutawapangia wapi wanatakiwa kwenda kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba pindi madaktari hawa watakapomaliza masomo yao basi Mkoa wa Irinnga utakuwa ni moja ya mikoa ambayo tutawapa kipaumbele. Hawa madaktari ambao amewaongelea ni madaktari wa kipaumbele ambao na sisi tumeweka msisitizo kuhakikisha kwamba tunawapa mafunzo na hospitali zote za Rufaa za Mikoa zinakuwa na madaktari bingwa hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ameuliza ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba tunaongeza rasilimali watu. Ni kweli hili jambo tunalo na katika mwaka huu ambao unaisha sasa, Serikali imeajiri watumishi zaidi ya 11,000 kuziba mapengo mbalimbali ambayo yamekuwepo na ajira mpya. Serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais (TAMISEMI) pamoja na Ofisi ya Rais (Utumishi), tunaendelea kufuatilia vibali kuhakikisha kwamba tunapata wataalam wa afya kwa ajili ya maboresho makubwa ambayo tumeyafanya kwenye vituo vya afya na ujenzi wa hospitali za Wilaya ambazo tunaendelea kuzijenga kwa sasa kote nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na changamoto hii ya watumishi, kwa kweli watumishi wetu wa afya wanafanya kazi kubwa sana na nzuri katika kuwahudumia Watanzania. Rai yangu katika mikoa yote ikiwa ni pamoja na Mkoa huu wa Iringa ni kuhakikisha kwamba viongozi wa Serikali na viongozi wa vyama wanatengeneza mazingira wezeshi kuhakikisha kwamba watumishi ambao tunawapeleka kule basi wanatengenezewa mazingira wezeshi ya kuweza kufanya kazi zao vizuri.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, napenda kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, je, ni kwa nini miji inapopanuliwa maeneo ya mashamba ya mazao marefu yasiachwe mijini kama ilivyo katika nchi nyingine kama Malaysia ambapo kilimo cha michikichi na mazao mengine kinaendeshwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, sheria hiyo haihusishi baadhi ya Mikoa kama Kagera, Kilimanjaro na Arusha ambako wakulima wanaendelea kulima mijini mazao marefu?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kama nilivyotoa majibu ya swali la msingi, Serikali huwahamisha wakulima wa mazao ya aina zote kwenye maeneo ya mijini yaliyoiva kwa ajili ya ukuaji au uendelezaji wa miji kwa kuzingatia Sheria ya Mipango Miji, Na. 8 ya 2007 (Kifungu cha 7 na Kifungu cha 28 na Kanuni zake za mwaka 2008. Sheria hii hutumika kwa pamoja na Sheria ya Utwaaji wa Ardhi, Na. 47 ya 1967; Sheria ya Ardhi, Na. 4 ya 1999 na Sheria ya Upimaji na Ramani, Sura ya 324 ya mwaka 2002.

Mheshimiwa Spika, hivyo, sheria za nchi yetu zinazohusika na usimamizi wa uendelezaji wa miji haziruhusu uwepo wa mashamba ya mazao marefu mijini isipokuwa sheria hizo zinaruhusu kilimo cha mijini (urban farming) cha mazao mafupi yasiyozidi urefu wa mita moja hususan kilimo cha mboga mboga.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, sheria tajwa katika majibu niliyoyatoa katika swali la kwanza la nyongeza hapo juu zinatumika katika maeneo yote ya nchi yetu ya Tanzania na hivyo sheria hizi hazitumiki kwa kubagua baadhi ya mikoa fulani ya Tanzania. Sehemu kubwa ya mazao marefu yanayolimwa katika Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Kagera ambayo ni kahawa, migomba na miparachichi yana sifa ya kuhifadhi mazingira na kupendezesha mandhari ya miji na makazi kama ilivyo kwa miti ya vivuli na matunda.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza, kabla sijauliza kwanza nikushukuru Mheshimiwa Naibu Waziri nimekuwa nikikusumbua sana kwa masuala ya afya, Mkoa wetu wa Iringa na wakati wote upo tayari. Naomba sasa nikuulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kukosekana kwa kipimo hiki katika hospitali yetu ya Mkoa wa Iringa kumefanya wagonjwa wetu kupata matatizo makubwa na mateso makubwa kwa sababu ni lazima kwanza waje wafanye kipimo Hospitali ya Mkapa au Hospitali ya Muhimbili Dar es Salaam. Kwa wagonjwa wasio na uwezo wamekuwa wakipata mateso na kusababisha vifo vingi sana katika mkoa wetu wa Iringa.

Je, Serikali sasa iko tayari kuhamasisha sekta binafsi kwa kutumia miradi ya PPP ili iweze kufunga katika hospitali zetu kwa sehemu ambazo hakuna mashine hizo?

Mheshimiwa Spika, swali letu la pili, kwa kuwa kumekuwa na mfumo usio mzuri kati ya MSD, hospitali na vituo vyetu vya afya kuletewa madawa yasiyoombwa na kuacha yale ambayo wanayaomba. Je, Mheshimiwa Waziri anaweza akalizungumziaje suala hili la madawa katika hospitali zetu na vituo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa sababu si tu amekuwa akieleza matatizo ya afya yaliyoko kwenye Mkoa wa Iringa, lakini vilevile amekuwa akiyazungumzia matatizo ya watumishi wa Mkoa wa Iringa.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tunaenda kwenye utaratibu wa bima ya afya kwa wote, lakini Serikali ina utaratibu wa PPP. Sasa kwa kuunganisha hayo kwa sababu utaratibu wa PPP unahitaji umakini wake kutekeleza tusubiri wakati tutaona jinsi ya kufanya namna tuweze kuona namna gani ya kushirikiana na private sector ili kufunga mashine hizo kwenye hospitali zetu, lakini ieleweke tu kwamba Serikali bado ina mpango huo wa kufunga kwenye hospitali zote, na sasa hapa tulipo kuna mashine mbili ziko njia kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni kwamba ameuliza kuhusu MSD, nalichukua wazo lake, ni wazo nzuri ambalo sasa Meneja wa MSD ataenda kulifanyia kazi kuhakikisha mawazo yake haya mazuri yanafanyiwa kazi kuhakikisha vinavyoagizwa ndivyo hivyo vinavyopelekwa kule. Lakini tunawaagiza Waganga Wakuu wa Mikoa na ma- DMO wote (Waganga Wakuu wa Wilaya) wahakikishe wanaweka takwimu sahihi za magonjwa ili wanapokuwa wanaagiza wafamasia waagize vitu kwa uhitaji wa hospitali husika bila kuagiza kwa namna nyingine tofauti.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, ndani ya wiki hii tuhakikishe tutatimiza ile ahadi yetu ambayo ilivunjika, twende Iringa tukakae pamoja, tujenge uelewa wa pamoja tuje tutatue matatizo ambayo Wabunge wote wa Mkoa wa Iringa wamekuwa wakizungumzia dawa hasa na vilevile na Mbunge wa Iringa Mjini, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa tatizo la ubakaji katika Mkoa wetu wa Iringa limekithiri sana; na kwa kuwa, tunaona kwamba, wanaobaka mara nyingi wamekuwa wakiweka Mawakili tena wasomi kwa ajili ya kutetea hizo kesi, matokeo yake wanashinda; na wale wanaobakwa kwa sababu, hawana uwezo walio wengi tumeona mara nyingi hata kesi zikienda wanashindwa. Je, Serikali inasaidiaje kuhakikisha wale watu wanapata haki zao, na hasa watoto wetu wanaobakwa?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri amejibu maswali ya kwanza kwa ufasaha sana. Jambo kubwa ambalo Serikali tumeendelea kusisitiza ni watu wetu kutokuyamaliza haya masuala kwa namna ya kindugu ama kirafiki na kuficha ushahidi, lakini kwa kile kipengele alichosema kwa wale watu ambao hawana uwezo wa kutafuta Mawakili tumetengeneza ule utaratibu wa msaada wa kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuko kwenye hatua za mwisho za kuzungumza kati ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ili kuweza kuanza kuwatumia Wanasheria popote pale walipo hapa nchini, wale walioko chini ya halmashauri, wale walioko chini ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, waweze kuwasaidia wananchi wale wasioweza kupata Mawakili kuwapatia msaada wa kisheria kama ambavyo viongozi wetu wakuu wamekuwa wakionesha mfano punde wanapofika katika eneo ambako kuna wananchi wana kilio, wamekuwa wakiingilia kati kuweza kuwasaidia, ili waweze kupata msaada huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshajaribisha sehemu mojawapo tulipokuwa na suala moja la mwananchi mmoja ambaye hakuweza kupata suala la wakili, lakini pia hakuweza kujua masuala ya kisheria, kuweza kusaidiwa na Wanasheria waliopo Ofisi za Mkuu wa Wilaya ama Ofisi za Mkurugenzi kwa maelekezo ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye Wanasheria wote Mawakili wako chini yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la muuliza swali ni la msingi kwa sababu kwa wakati mwingine hata mwananchi akiwa na Wakili kumekuwa na utaratibu wakati mwingine Mawakili wanazungukwa na wale watenda maovu, I mean wale Wanasheria, kama mlalamikaji hana fedha wanaweza wakazungukwa na wale wenye fedha ikatokea wakashindwa kupata haki yao. Kwa hiyo, tutakapokamilisha hili, tangazo rasmi litatoka ili wananchi waweze kupata haki zao.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa ili tatizo la mlundikano wa pikipiki kwenye Vituo vya Polisi liko katika mikoa mingi, lakini utaona vijana wengi ambao wanakamatwa kuna wengine ambao hawana makosa yale ya kusema kwamba pikipiki ziwekwe kituoni. Hata hivyo, kuna wengine wameenda kukopa benki ili kama ni ajira kwa vijana, sasa wasema kwamba lazima miezi sita. Sasa ni kwa nini kusiwepo na kitengo maalum kwa sababu limeonekana hili ni tatizo karibu nchi nzima, cha kushughulikia hili tatizo la ukamataji wa bodaboda ili pengine kipindi kiwe kifupi miezi miwili au mitatu kwa sababu mengine ni makosa ambayo sio makubwa sana ya kuweka mpaka miezi sita na wengine wamepata ajali wamekufa na wengine wako hospitali? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana yaliyotolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Mheshimiwa almaarufu Chilo, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kabati, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kumekuwa na matukio ya mengi yanayotakana na namna ya uendeshaji wa biashara yenyewe ya bodaboda lakini pia industry nzima hiyo ukilinganisha na hatua zinazochukuliwa katika kupambana katika kuweka utaratibu wa kufuata sheria katika kufanya biashara yenyewe ifanyike lakini pia usalama wa watu.

Mheshimiwa Spika, moja kati ya vyombo vinavyotumika sana kwa sasa kufanya uhalifu ni pikipiki kuliko hata magari na kwa hivyo kumekuwa na sababu tofauti tofauti ambazo zinapelekea ukamataji na wenyewe kuwa mkubwa. Wengine wengi ni rahisi akienda kufanya tukio lenye thamani kubwa au akapora au akafanya nini kuitelekeza pikipiki ni jambo jepesi, kwa hiyo tunajikuta tuna pikipiki nyingi ziko mikononi mwa polisi, lakini wahusika ama hawajulikani walipo wamezitelekeza na ndio maana zinaitwa mali zilizookotwa.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, kwa sababu concern ya Waheshimiwa Wabunge ni kubwa kwenye jambo hili na kwa sababu pengine sababu hizi tatu zilizotolewa katika jibu letu la msingi zinaonekana hazikuwatosheleza Waheshimiwa Wabunge, acha tukafanye tathmini ya kina na tutakuja na matokeo haya tueleze kwa kina katika pikipiki zilizokamatwa nchi nzima zilizopo kwenye Vituo vya Polisi ni ngapi; na ngapi zina tatizo gani na ngapi zina tatizo gani.

Mheshimiwa Spika, kwa hatua ya muuliza swali la msingi kwamba tuone utaratibu wa kuzi-dispose kwa sababu tumesimamisha uchumi na yenyewe ni hoja ambayo ni valid. Tutakachokifanya katika tathmini hiyo tutaona kama tutapata wale waliopo husika, ili tuweze kuzipiga mnada. Kwa hiyo, nadhani tupewe muda, twende tukafanye tathmini ya jambo hili na baadaye tutoe matokeo yake hadharani.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu ya Serikali. Naomba niulize maswali madogo mawili. Kutokana na Mradi huu wa REGROW tulitegemea sasa wananchi wa Mikoa ya Kusini kuanza kutengeneza ajira nyingi sana kupitia utalii na kuongeza pato la mikoa hii; na tulitegemea sasa ujenzi wa Vyuo vya Utalii Nyanda za Juu Kusini katika eneo la Kihesa Kilolo na Makao Makuu.

Je, ni elimu kiasi gani imetolewa kwa wananchi wa mikoa hii ili kuwajengea uwezo katika kuupokea mradi huu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Biashara ni matangazo. Kwa kuwa mikoa yetu hii ya kusini tunavyo vivutio vingi na vizuri vikiwemo Mbunga za Wanyama Ruaha National Park ambapo ni Mbuga ya pili kwa ukubwa katika Afrika; tunavyo vivutio vingine kwa mfano pale Kihesa kuna Gangilonga, jiwe lililokuwa linaongea, lakini tuna Kitanzini ambayo ni sehemu ambayo watu walikuwa wanajinyongea; na vile vile tunalo fuvu la Mtwa Mkwawa ambalo lipo pale Kalenga…

SPIKA: Sasa swali Mheshimiwa.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nini mkakati wa kuvitangaza hivi vivutio vya kusini ili kupata angalau tupate watalii wa ndani na kuongeza mapato? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Ritta kwa swali lake zuri, maana hii ni kwa manufaa ya Mikoa yote ya Kusini mwa Tanzania. Mradi huu ni faida kubwa sana kwa wananchi na mikoa ya kusini mwa Tanzania kwani Serikali imewekeza kiasi kikubwa cha fedha ambao ni mkopo.

Mheshimiwa Spika, katika swali la msingi la Mheshimiwa Ritta ameuliza kwamba tuna mkakati gani kuhakikisha wananchi wanapata elimu ya kutosha pindi wanapopokea huu mradi? Pia na namna ambavyo wataenda kutelekeleza.

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ina mpango mkubwa wa kuanzisha vyuo ambavyoo vitakuwa ni campus. Tunaanzisha campus ya Mweka na pia kutakuwa na Chuo cha Mambo ya Utalii ambacho kitaanzishwa kama Campus ya Iringa. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi kwamba wananchi wa kusini mwa Tanzania wataweza kuelimika. Pia tutahamasisha utalii kupitia elimu hiyo.

Mheshimiwa Spika, swali lake lingine alisema biashara ni matangazo. Ni kweli bila kutangaza vivutio vyetu tulivyonavyo hapa nchini, utalii hauwezi kuendelea. Kipindi cha mpango huu wa bajeti, tumetenga kiasi cha shilingi bilioni 46.5 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba utangazaji wa vivutio tulivyonavyo hapa nchini unafanyika kwa nguvu zote.

Mheshimiwa Spika, pia kwenye utangazaji bila kuimarisha miundombinu inakuwa ni changamoto; na hilo nimtoe wasiwasi kwamba tumetenga shilingi bilioni 75.4 ambazo zitaimarisha miundombinu iliyoko kwenye hifadhi hizo ili tuimarishe na kutangaza kwa bidii. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini niseme kwamba Hospitali ya Frelimo ilijengwa ili kupunguza msongamano mkubwa sana uliopo katika Hospitali yetu ya Mkoa na mpaka sasa hivi tunashukuru kwamba tumeweza kupata milioni 500, lakini hakuna hata wodi moja toka mwaka 2012 imeanzishwa, lakini pia tushukuru kwa hizi shilingi milioni 400 ambazo tumepewa kwa ajili ya kujenga majengo ya maabara na uchunguzi.

Sasa ni lini Serikali italeta vifaa kama vya X-Ray, MRA, CT Scan ili sasa wananchi wa Iringa wasiendelee kwenda kwenye Hospitali ya Mkoa?

Mheshimiwa Naibu Spika, Swali langu la pili, Sera ya Serikali ni kujenga vituo vya afya kila kata. Lakini Manispaa yetu ya Iringa ina kata 18 na ina vituo viwili tu vya Ngome na Ipogolo, vituo ambayo kwa kweli ni vichakavu mno na havijawahi kufanyiwa ukarabati wowote toka vimeanzishwa. Na tulitegemea kwamba hivi vituo…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ritta Kabati uliza swali.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Kuna population karibu ya watu laki mbili.

Je, ni lini Serikali sasa hivi itaboresha hivi vituo vya afya ili viweze kufanya huduma ya upasuaji ili kupunguza msongamano mkubwa uliopo katika Hospitali yetu ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru kwa kutambua kwamba Serikali imeendelea kuwekeza fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Hospitali hii ya Manispaa ya Iringa - Frelimo inatoa huduma na kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimhakikishie kwamba, kama ambavyo tumeweka katika mipango yetu katika mwaka wa fedha ujao tutaendelea kutenga fedha kwa awamu ili kuhakikisha wodi zote katika hospitali ile zinajengwa, zinanakamilika ili ziweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi wa Manispaa ya Iringa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nimhakikishie kwamba vifaa tiba ni moja ya kipaumbele cha Serikali na ndio maana katika bajeti yetu 2021/2022 tumetenga zaidi ya shilingi bilioni 14 kwa ajili ya kununua vifaa tiba katika vituo vyetu na hospitali zetu. Kwa hiyo, nimuhakikishie hospitali hii pia itapewa kipaumbele kuhakikisha kwamba tunakwenda kupeleka vifaa tiba katika hospitali ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tatu kuhusiana na vituo vya afya tutaendelea kujenga na katika mwaka wa fedha ujao Manispaa ya Iringa ni moja ya Manispaa ambazo zitajengewa vituo vya afya.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa, sera ya Serikali ni kuunganisha kwa kiwango cha lami barabara za Mikoa na Wilaya na kwa kuwa barabara ya Idete – Iringa ni barabara ambayo inaunganisha Majimbo matatu, Iringa Mjini, Jimbo la Kalenga na Jimbo la Kilolo.

Je, ni lini sasa Serikali itaijenga kwa kiwango cha lami barabara hii kwa sababu kwanza ni ya kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA
M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum maarufu wa Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba barabara aliyoitaja ni muhimu sana, na mpango wa Serikali ni kuunganisha mkoa na mkoa na wilaya na wilaya.

Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwa niaba ya Serikali, kwamba fedha zikipatikana wakati wowote barabara hizi zote muhimu zitajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante sana.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ajali inapotokea wamiliki wa vyombo vya moto hupewa mara moja bima yao wanapokwenda kudai chombo kama imeharibika, lakini hawa waathirika ambao ni abiria wanaopata ajali wamepoteza maisha au viungo wamekuwa wakisumbuliwa sana na hawa bima.

Je, nini kauli ya Serikali kutokana na usumbufu mkubwa sana wanaopata abiria wanaopata ajali barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa abiria wengi sana wanaotumia vyombo vya moto wanapopata ajali wanakuwa hawana uelewa wa kutosha na mara nyingi sana sasa hivi tumetumia electronic ticketing yaani kule nyuma hakuna elimu yoyote.

Je, sasa Serikali haioni ni wakati sasa wa kuhakikisha kwamba katika vituo vya kusubiria abiria kuwepo na mabango na matangazo ili kutoa elimu ya kutosha kwa abiria wanapopata ajali nini wafanye? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Iringa.

Kwanza nataka nichukue fursa hii nimpongeze sana kwa kazi nzuri ambayo anaifanya katika Mkoa wake. Mheshimiwa Ritta amefika hatua ya kukarabati Kituo cha Polisi na ujenzi wa kumalizia Kituo cha Polisi katika Kata ya Semtema. Hakika amefanya kazi kubwa, kwa hili nampongeza sana lakini na wengine pia watusaidie kufanya hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niombe kujibu maswali mawili. Inapotokea ajali ni kweli mmiliki wa chombo anapata fidia kama amejiunga ama amejihusisha na bima, lakini je vipi kuhusu sasa hawa abiria. Ni kweli hii ni changamoto na bado kuna changamoto nyingine kwa upande wa wananchi. Hapo nataka niwaambie kitu kwamba changamoto ya kwanza wanapopata ajali wanakuwa hawajui namna bora ya uandishi wa barua za kuombea zile fidia zao, kitu ambacho mwisho wa siku kinakuja kuwafanya wao aidha kuchelewa au kukosa kabisa kuweza kupata zile fidia kutoka bima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine kwa kweli ipo kwenye upelelezi kwamba wale watu wa bima hawawezi kutoa zile fedha za fidia unless mpaka wahakikishe kwamba wamepata attachment ya upelelezi kutoka Jeshi la Polisi. Kwa hiyo, hapo nataka nitoe wito pia kwa Jeshi la Polisi kwamba wahakikishe wanafanya haraka kupeleka ripoti za upelelezi kwa hawa wananchi ambao wanapata ajali ili sasa waweze kupata fidia zao kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kikubwa zaidi uelewa mdogo wa hii taaluma ya bima. Hapa natala nitoe agizo kwa Jeshi la Polisi, kwamba pamoja na kazi nzuri ya utoaji wa elimu kwa wananchi juu ya namna bora ya utumiaji wa barabara, lakini suala la elimu hii ya bima ya kuweza kupata mafao iendelee na kazi ifanyike vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine alikuwa anauliza je, sasa tuna mpango gani wa kuweka haya mabango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabango yapo, kazi imeanza na inaendelea, lakini kingine tunaendeleza taaluma ambazo kupitia mabango, vyombo vya habari, vijiwe vya bodaboda, shule pamoja na kupitia kila mahala; tunawaelewesha watu namna bora ya kutumia barabara na kuepuka na ajali. Kikubwa zaidi tumeshaweka ishara na alama za barabarani ambazo pia zinasaidia watu kuweza kujua namna ya kuepuka hizi ajali za barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali.

Kwa kuwa tatizo la masoko liko pia katika mazao mbalimbali nchini na kwa kuwa sasa hivi, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuweka kitengo cha kutafuta masoko katika Balozi zetu, ili kiweze kushughulikia tatizo la masoko katika mazao mbalimbali nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa tayari Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeunda Idara maalum ya Economic Diplomacy, kwa ajili mahsusi ya kutafuta masoko ya bidhaa zetu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyoneza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nilikuwa naomba kuuliza. Katika mkoa wetu wa Iringa bado kuna maeneo ambayo yanasuasua katika mawasiliano na hasa katika ya Nyazwa, pamoja na kuwa kuna mnara wa Halotel lakini bado kabisa maeneo mengi sana hakuna mawasiliano. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba Mkoa wote wa Iringa kata zote zinapatiwa mawasiliano ya kutosha?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati Mbunge wa Viti Maalum kutoka Iringa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba inafikisha mawasiliano kwa wananchi wote na kuhakikisha kwamba tunaimarisha upatikanaji wa mawasiliano. Lakini naomba kupokea changamoto hii ili tuweze kutuma wataalamu wetu wakafanya tathmini na ili wajiridhishe kchangamoto iko na ukubwa gani ili tuchukue hatua stahiki. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulizie maswali mawili.

Kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake lakini pia niwapongeza Watanzania kwa michango mizuri ambayo wamechangia nchi yetu wanaoishi nje ya nchi. Kwa kuwa Diaspora wakirudi nchini huwa wanachukuliwa kama wageni kwenye nchi yao.

Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kutoa hadhi maalum kwa Diaspora kushiriki ujenzi katika uchumi na uwekezaji kabla hatujaweza kupewa uraia pacha?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; je, watanzania wanaoishi nje ya nchi wanapopata matatizo kwa mfano kesi, wamekuwa wakipatiwa msaada gani ukiwepo msaada wa kisheria?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge ambaye ni mdau mkubwa sana wa diaspora kwa namna anavyowasemea na kuhakikisha fursa nyingi kwa wana diaspora. Wizara yetu kwa kushirikiana na taasisi za Serikali zote mbili za Tanzania Bara na Zanzibar na kwa kushirikiana na wadau wa sekta binafsi wanaoshughulika na mambo ya Diaspora tayari imeanza kufanya tafiti ili kupitia sera, sheria na taratibu za nchi kwa ajili ya kuangalia uwezekano wa watanzania wanaoishi nje kupata hadhi maalum.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la pili la msaada wa kisheria wakati wanapopatwa na matatizo kama vile kesi ni kwamba Serikali kupitia balozi zetu zimekuwa zikiwasaidia watanzania wanapopatwa na kesi nje ya nchi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kuwatafutia mawakili mabobezi na waaminifu kwa gharama zao; pili, pale kesi inapokuwa katika Mahakama ubalozi umekuwa ukifuatilia kwa karibu sana kesi hizo ili kuona watanzania hawa wanapata haki zao kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi husika.

Mheshimiwa Spika, mwisho pale wanapomaliza vifungo vyao au wanapopata msamaha ubalozi unafanya uratibu wa kuhakikisha kwamba wanarudi nyumbani salama, ahsante sana. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa, tatizo la afya ya akili hata katika Mkoa wetu wa Iringa limekuwa kubwa sana na changamoto kubwa kabisa ya tatizo hili ni kwamba, bei ya dawa iko juu sana, sana. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba, dawa zinakuwa na bei ndogo au kuondoa kabisa, ili waweze kupatiwa bure kama yalivyo magonjwa mengine?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba nijibu swali lake la nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwanza dawa za wagonjwa wa akili zinatolewa bure na tayari Serikali imeshapeleka kwenye maeneo yote watu wa kufanya hivyo. Kama kuna mahali wanawauzia kwa Mkoa wa Iringa, nitalifanyia kazi ili kuona namna ya kufanya. Nalipokea ili tuweze kulifanyia kazi. Wote tutaona kwamba Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ameshaunda Wizara ya Maendeleo ya Jamii, mojawapo ya kazi ni kuhakikisha, ile Wizara itakaposimama kwenye eneo lake tutapunguza sana mambo yanayosababisha yanayoongezea idadi ya watu wenye matatizo ya akili kwenye jamii.

Kwa hiyo, kikweli nachukua wazo la Mheshimiwa la dawa, lakini tutaenda kulifuatilia zaidi na kwenda Iringa kuimarisha zaidi hicho kitengo ambacho umekizungumzia hasa kwenye eneo la dawa.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa maswali madogo mazuri ya nyongeza. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini mradi wa barabara inayounganisha Jimbo la Iringa Mjini, Jimbo la Kalenga na Jimbo la Kilolo utakamilika? Kwa sababu mradi huo ni wa siku nyingi sana na wakati wa mvua wananchi wanapata mateso makubwa na barabara hiyo ni ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ni lini mradi wa barabara ya Msembe inayokwenda Ruaha National Park utakamilika? Kwa sababu barabara hiyo pia ni ya kiuchumi na inakosesha mapato makubwa sana kwa Serikali kwa kuingiza mapato ya watalii wa ndani na wa nje. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na jibu la barabara ya Ruaha National Park; barabara hii ipo kwenye bajeti na iko kwenye taratibu za manunuzi. Hali kadhalika barabara ya Iringa kwenda Kilolo inaendelea kujengwa na tuna hakika kadri fedha zitakavyopatikana barabara hii ni azma ya Serikali iweze kukamilika kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na nishukuru sana majibu ya Naibu Waziri japokuwa yamekuwa ni hayo hayo muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo katika muingiliano huu wa hospitali na magereza kwa kweli unatesa sana wananchi wa Mkoa wa Iringa. Kiasi kwamba barabara ile imefungwa ambayo inaingilia hospitali kuna wakati wafungwa wakitolewa, ambulance inashindwa kupita inazunguka mzunguko mrefu sana kumuwahisha mgonjwa hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kuwa tulipokaa katika kikao cha Mkoa - RCC iliazimia kwamba kwa sababu hii changamoto haitatuliki basi tuiombe Serikali either ibadilishe kwamba majengo yaliyopo katika hospitali hii yawe hospitali ya wilaya na eneo ambalo lipo Frelimo kwa sababu ni kubwa sana linaweza likajengewa hata nyumba za madaktari basi iwe ndio hospitali yajengwe majengo ya hospitali ya mkoa. (Makofi)

Je, sasa Mheshimiwa Waziri yupo tayari kushirikiana na Wizara ya Afya ili kuona changamoto hii iweze kuondoa tatizo lililopo katika Mkoa wetu wa Iringa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; sambamba na hilo kwa kuwa katika Mkoa wetu wa Iringa pia lipo Gereza Kihesa Mgagao, Wilaya ya Kilolo, hili eneo ni eneo ambalo walikaa wapigania uhuru wa South Africa - ANC lakini utaona wenzetu walipokaa…

SPIKA: Mheshimiwa Ritta uliza swali.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ndio.

Mazimbwi, Dakawa wamejenga vituo vya maendeleo kama shule hospitali lakini eneo hili bado kuna Gereza…

SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa Ritta.

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, je, Serikali sasa kwa sababu tulikuwa tumeomba pia hilo Gereza lihamishwe ili kijengwe hata Chuo cha VETA… (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt. Kabati kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza Wizara yangu iko tayari kuwasiliana na Wizara ya TAMISEMI na Wizara ya Afya ili kuona uwezekano wa kuhamisha mojawapo ya huduma kutoka Hospitali ya Mkoa iwe Hospitali ya Wilaya halina tatizo kabisa.

Mheshimiwa Spika, lakini hili la pili nadhani halikukamilika swali lenyewe kwa hiyo, nashukuru sana. (Makofi/Kicheko)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na sheria za ndoa, lakini kuna tatizo kubwa sana la malezi kwa watoto wetu. Kuna changamoto kubwa sasa hivi ya wazazi kuwapeleka watoto wadogo kuanzia nursery school mpaka sekondari katika shule za boarding na watoto kukosa malezi ya wazazi. Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha sasa mitaala inarudishwa kwa mfano ile ya sayansikimu katika shule zetu ili watoto waweze kupata malezi na kupata elimu za kujitegemea?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimkiwa Dkt. Ritta Kabati la nyongezab kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumepokea hoja yako. Ni kweli, kuna kasi kubwa ya mmomonyoko wa maadili inayoendelea na inasababisha masuala mengi sana ya visa vya ukatili. Kwa sababu marekebisho ya mitaala yanaangukia sekta nyingine tumelipokea tutakwenda kukaa tulijadili kwa pamoja, tujange hoja tuone namna gani tunaweza tukafanya ili kurekebisha hiyo mitaala ikidhi na kuakisi changamoto za sasa kwa ustawi wa Taifa letu la kesho.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Ninamshukuru kwanza majibu ya Mheshimiwa Waziri lakini changamoto kubwa kuna baadhi ya Vijiji, Kata hakuna hospitali wala vipimo, sasa sijui anawasaidiaje wazazi ambao wanazaa watoto wachanga ambao wapo katika vijiji ambavyo hakuna hata hospitali yenye vipimo kama hivyo?

Swali langu la pili, kuna watoto ambao wanazaliwa na sickle cell wamekuwa wakipata mateso makubwa sana, damu kupungua mwilini, lakini sasa hivi tunaona kwamba hatupatiwi dawa bure katika hospitali zetu. Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba wanawasaidia watoto wanaozaliwa na sickle cell?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo.

Moja ni suala la kwamba kuna watoto ambao vituo haviko kule, ndiyo maana kuna juhudi kubwa ambayo Rais wetu anafanya kwenye masuala ya kujenga vituo vya afya kila mahali katika nchi yetu na ndiyo maana pia tunasisitiza kila mama mjamzito aweze kujifungulia kwenye zahanati au kituo cha afya ili utambuzi uweze kufanyika na kumpa mtoto tiba stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili linalohusu suala la selimundu maana yake sickle cell ni kweli kuna tatizo hilo katika nchi, lakini imeshachukuliwa hatua sasa na dawa ya kuweza kuwasaidia hawa watoto imeshawekwa package yake kwa ajili ya kununuliwa na MSD na kusambaza kwenye vituo vyetu na kuweka utaratibu maalum, kwa kushirikiana vilevile na Serikali ya Marekani tayari vilevile imetengenezwa program maalum ambayo inashughulikia watoto wenye matatizo hayo. Ahsante sana.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, kutokana na mabadiliko ya tabianchi mipaka mingi ya asili baina ya mikoa na mikoa, wilaya na wilaya, kata kwa kata, vijiji kwa vijiji, vitongoji kwa vitongoji imebadilika sana.

Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha sasa Mipaka hiyo ili iwe sawasawa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali letu la pili. Je, ni nili huo mradi wa Korea utaanza?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza yaliyoulizwa na Mheshimiwa Ritta Kabati kwa niaba ya Mheshimiwa Angelina Malembeka kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kuhusiana na jambo la tabianchi, ni kweli ipo baadhi ya mito ya asili ambayo imekauka hivyo kusababisha migogoro katika baadhi ya maeneo. Hata hivyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na kulihakikishia Bunge lako kwamba Serikali imeshafanya zoezi la kutambua na kuchora ramani za mikoa hiyo, hivyo suala hilo litakapokuwa limetokea zipo hatua ambazo zimeshachukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, juu ya ni lini mradi utaanza, nataka kulihakikishia Bunge lako kuwa, pale tutakapokuwa tumeshaandaa taratibu zote, ikiwemo kuweka ofisi na kupata wataalam wakaosimamia zoezi hilo, zoezi hilo litaanza.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa ukatili huo upo nchi nzima, kwa nini vituo hivi vimejengwa katika mikoa miwili tu yaani Dodoma vituo 20, Dar es Salaam vituo 10, ilhali changamoto hii ipo nchi nzima ikiwepo Mkoa wetu wa Iringa?

Mheshimiwa Naibu Spika, je, Wizara hii sasa haioni haja ya kushirikiana a Wizara ya Elimu ili kuwa na shule maalum zitakazotoa msaada kwa watoto walioathirika na ukatili huo kama ilivyofanyika katika programu ya MEMKWA?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu hivi vituo 30 vilivyoanzishwa vilikuwa ni vituo vya awali vya majaribio ili kutuwezesha kuona jinsi mfumo unavyofanya kazi. Kwa sasa tumeshaona na tayaru tuko kwenye maandalizi ya mwongozo wa jinsi ya kuvianzisha na kuviendesha nchi nzima, katika mikoa yote. Tunatarajia mapema mwakani mwongozo ukamilike ili tuende nchi nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili kuhusu kuufanya mfumo tuwe kama mfumo wa MEMKWA katika suala zima la kuwafundisha hawa watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo uliopo unafanya kazi vizuri kiasi kwamba mtoto anapokutwa na matatizo anapata huduma za kisheria, kisaikolojia, kiafya, chakula na tunamrejesha kuendelea na maisha. Ikitokea sasa kuna tatizo lingine linalozuia asiendelee vizuri tunawapeleka kwenye nyumba salama makao ya watoto na hapo tunaungana na Wizara ya Elimu kutafuta aendelee shule gani tofauti na ile ya awali. Hivyo basi, tumepokea maoni kama itabidi iwe hivyo tutajadili na Wizara ya Elimu kwa nyakati zijazo tuone jinsi ya kufanya, lakini sasa hivi mfumo unafanya kazi vizuri.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tulipokuwa tunafanya elimu ya sensa katika Mkoa wetu wa Iringa kuna baadhi ya vijiji wana vijiji kabisa hawajui kabisa kama wanapataje namba za utambulisho, na kuna baadhi wana namba za utambulisho muda mrefu sana hawajapatiwa NIDA.

Je, ni lini sasa waliopata namba watapata na wale ambao hawajasajiliwa watapata angalau elimu wajue wanasajiliwaje?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna haja ya kuongeza jitihada za kutoa elimu kwa wananchi kuhusiana na huduma hii ya vitambulisho na katika kufanya hivyo kuna njia kadhaa. Njia moja ni kuhakikisha kwamba huduma hizi zinasogea karibu na wananchi. Katika kufanya jitihada hizo, Serikali imefanya kazi kubwa sana kuhakikisha inaimarisha Ofisi za NIDA katika ngazi za chini kwa maana ya Wilayani ili Maafisa hawa wa NIDA waweze kuwa karibu na wananchi na waweze kutoa huduma ikiwemo hii huduma ya Elimu kwa Umma.

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza hilo, katika bajeti ya mwaka huu tunatarajia kuongeza ujenzi wa vituo zaidi 31 katika wilaya 31 nchini. Lengo ni kuhakikisha kwamba Wilaya zote katika nchi hii zinapata huduma ya NIDA ili kuwa karibu na wananchi waweze kupata huduma mbalimbali ikiwemo elimu itakayowezesha kuwasaidia kujua haki zao za msingi katika kupata kadi na vitambulisho vya NIDA kwa ujumla wake.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri kwamba Mkoa wetu wa Iringa na sisi tuna madini ya kutosha. Mkoa wetu wa Iringa tunao Mgodi wa Nyakavangala uko katika Jimbo la Isimani. Na kwa kuwa taarifa ya jiorojia na utafiti, inaonesha kwamba eneo hilo limeshaonesha. Je, ni hatua gani sasa inayofuata ili wachimbaji wa eneo hilo waweze kuchimba kwa tija na ili Mkoa wetu wa Iringa uweze kupata mapato kutokana na madini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nipongeze sana wanawake waliothubutu kuanza uchimbaji wa madini nchini, na sasa wameanzisha chama cha TAWOMA. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhamasisha wanawake wengi zaidi waweze kuchimba madini nchini na ukizingatia sensa inaonesha kwamba wanawake tuko wengi zaidi na Mheshimiwa Waziri alisema tunalipa vizuri?

Nimpongeze Mheshimiwa Rais alifungua uwekezaji mkubwa sana wa mwanamke pale Geita, Sarah Masasi, ili wanawake wengi tuweze kuchimba madini na kuwekeza katika madini nchini. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa swali lake la kwanza kwamba kwa kuwa utafiti wa awali umeshafanywa na taasisi zetu kubaini uwepo wa madini ya dhahabu katika eneo la Nyakavangala, napenda kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kwamba hatua zinazofuata sasa ni kufanya utafiti wa jiofizikia ambao ndio unaohitajika kwa sasa ili usaidie kutambua mikondo inayoweza kuwa na mashapo ya dhahabu, na kwa njia hiyo wale wachimbaji waweze kuchimba kwa tija. Aidha, GST kwa kushirikiana na STAMICO sasa wamepanga kwenda kuendelea na utafiti katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa swali lake la pili, ni kwamba Serikali ya Mama Samia kwa kuzingatia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi unaotutaka tuwape wachimbaji wadogo wakiwepo wanawake maeneo ya kuchimba madini imetuagiza sisi tuendelee kuwa walezi wa sekta ndogo ya wachimbaji wakiwepo wanawake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika kutekeleza hilo sisi Wizara ya Madini, kwanza tumeteua mabalozi wa madini ambao Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati ni moja wa mabalozi na vinara wa madini hapa nchini, kazi ambayo anaifanya kwa dhati, na mpongeza kwa kuleta swali hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hivi mamia kwa maelfu ya wanawake wanafaidika kupitia mnyonyoro wa sekta hii ya madini. Zaidi ya leseni 20 zimeshatolewa kwa vikundi mbalimbali vya wachimbaji wa madini. Na wanawake hawa wamekuwa wakichangia pia katika kukusanya maduhuli ya Serikali. Kwa mfano kikundi kimojawapo cha TAWOMA mshikamano kilichopo katika eneo la Nyamisiga, Halmashauri ya Msalala kule Kahama wamechangia ujenzi wa zahanati. Hizo ni juhudi kuonesha kwamba Wizara imezingatia suala hili la uchimbaji wa wanawake wadogo, na ninampongeza sana Mheshimiwa kwa kuleta swali hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuwaomba wanawake popote walipo Tanzania kwenye madini wajiingize katika biashara hii maana ina tija na Serikali inawatambua na itawa-support.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Uwanja wetu wa Iringa ni uwanja ambao tayari umeshawekwa jiwe la msingi na Mheshimiwa Rais;

Je, ni lini sasa utakamilika kwa sababu ujenzi umechukuwa muda mrefu sana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uwanja huu unaendelea kujengwa lakini pia uwanja huu World Bank imekubali kuufadhili, na kwa kuwa unaendelea. Kama kulikuwa na changamoto za kuchelewa, nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kasi imeongezeka na tuna hakika uwanja utakamlishwa kwa sababu mkandarasi yupo site na anaendelea na kazi. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa katika Manispaa ya Iringa katika Kata ya Isakalilo kuna Mradi wa Mkoga katika Kata ya Kituli kuna Mradi wa Kitwilu. Hii miradi ni ya muda mrefu sana. Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kutoa pesa ili wananchi hasa akinamama na vijana waweze kujiajiri kupitia hii miradi kwa kulima mbogamboga na matunda?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika majibu yangu ya awali kwamba miradi yote hii na hasa katika Mkoa wa Iringa tumeshatenga fedha tayari kwa ajili ya Tume yetu kukamilisha kazi hii ya uhakiki. Bahati nzuri Mheshimiwa Rais ametuongezea bajeti kutoka shilingi bilioni 17 mpaka bilioni 51, nataka nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba katika kuelekea ajenda 1030 ya kukuza kilimo katika nchi yetu, moja ya kipaumbele ni kilimo cha umwagiliaji, hivyo hatutaacha mradi wowote nyuma, miradi yote tutajenga tukipata fedha ambazo zitatuwezesha kufikia malengo hayo.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, na ninamshukuru Mhehsimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri naomba niulize maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; ni lini Serikali itapeleka magari ya wagonjwa kwa Hospitali ya Ilongelo na Hospitali ya Wilaya ya Manyoni iliyopo Singida?

Mheshimiwa Spika, swali la pili vituo vya afya vya Ngome na Ipogolo vimekuwa vikitumia magari ya abiria katika kusafirisha wajawazito kwenda kujifungu. Ni lini sasa Serikali itaona umuhimu pia wa kutupatia magari katika hospitali yetu ya Wilaya ya Iringa Manispaa na katika vituo hivyo vya Afya vya Iringa Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu kwenye jibu langu la msingi, kwamba Serikali itanunua magari ya wagonjwa 195 kwa ajili ya Halmashauri zetu zote 184 nchini kote. Kwa hivyo Kituo cha Afya na Hospitali ya Ilongelo na Manyoni zitanufaika kwa magari hayo lakini bado tutaendelea kutenga fedha kwa awamu ili vituo vingine vyote vipate magari ya wagonjwa, kwa maana ya kuboresha huduma za rufaa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Ngumi, Ipogolo na Hospitali ya Manispaa ya Iringa ni kweli ina changamoto ya gari la wagonjwa; na Manispaa ya Iringa nayo itanufaika na magari haya. Kwa hiyo changamoto hiyo kwa sehemu itakuwa imetatuliwa, lakini tutaendelea kutafuta magari zaidi.

Mheshimiwa Spika, tarehe 06 juzi Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan amezindua mpango mkakati wa M-mama ambao utawezesha rufaa za dharura katika mikoa 12 kwa kushirikisha wadau, wakiwemo Vodacom. Kwa hiyo pamoja na jitihada za Serikali lakini bado jitihada za private sector kama Vodacom tutakwenda kuondoa kabisa changamoto ya rufaa kwa wagonjwa wetu, ahsante sana.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati maeneo mengine wanazungumzia habari ya ukarabati wa vituo vya Polisi, kwenye Mkoa wetu wa Iringa katika wilaya ya Kilolo bado Serikali haijajenga Makao Makuu ya Jeshi la Polisi ngazi ya wilaya ilhali ni zaidi ya miaka ishirini sasa Serikali imekuwa ikitoa ahadi.

Je, ni lini sasa Serikali itajenga makao makuu ya polisi Wilaya ya Kilolo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yaliyotangulia, ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba wilaya zote zinapata vituo vya polisi vyenye hadhi ya wilaya. Hivyo kutokana na upatikanaji wa fedha tunakwenda kwa awamu. Nimuahidi tu Mheshimiwa Ritta kwamba Wilaya ya Kilolo ni miongoni mwa wilaya zitakazozingatiwa hasa ukizingatia kwamba kuna uharibifu mkubwa wa mazingira yanayohitaji usimamizi wa sheria kwenye maeneo hayo. Kwa hiyo itapewa kipaumbele katika bajeti zetu.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Kinyanambo C - Mapanda hadi Kisusa katika Jimbo la Mufindi Kaskazini? Maana ilikuwa imeahidi kujenga kilometa tano tano na ni barabara ya kiuchumi.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, Iringa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja itajengwa kwa kiwango cha lami kufuatana na upatikanaji wa bajeti. Kwa hiyo, Serikali itaendelea kutafuta fedha kuijenga kwa kiwango cha lami barabara hiyo. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Kwa kuwa, changamoto kubwa kabisa inayokabili watu wenye ulemavu wanapokwenda hospitali hasa ni mawasiliano kati ya Daktari na mgonjwa, kwa sababu ulemavu unatofautiana.

Je, nini mkakati wa kuhakikisha kwamba Madaktari wanaelewa lugha za watu wenye ulemavu, kwa sababu wengine wanaongea kwa ishara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme Mheshimiwa kwa kweli ameelezea suala siyo tu kusema ulemavu lakini ni wenzetu wenye mahitaji maalum kwa sababu kila mmoja ana mahitaji yake tofauti ukilinganisha na mwenzake. Na anasema mojawapo ya sehemu ni kwenye mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli kwa mfano kwenye hospitali ya Kanda ya Mkoa wa Mbeya tayari tumeanza process ya kuweka wale watu wanaoweza kutafsiri lugha kwa ajili ya watu wenye mahitaji maalum, tunaendelea sasa ku-roll out kuingia kila mahali. Lakini kwa kweli kuna shida kubwa hasa kupata watu wale wenye uwezo wa kufafanua lugha, kufafanua na mambo mengine hasa inapofika maeneo ya kitiba. Lakini Serikali inawekeza eneo hilo nguvu kuhakikisha hao watu wanapata huduma hiyo.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, mimi nishukuru kwamba Serikali imeona hii changamoto kwa sababu katika Mkoa wetu wa Iringa hili tatizo ni kubwa sana, hasa kwenye hospitali yetu ya Mkoa wa Iringa wananchi wanasubiria kwenye magereza, kwa sababu hakuna kabisa eneo lakini pia katika Wilaya ya Kilolo Mufindi hakuna maeneo ya kusubiria wagonjwa.

Mheshimiwa Spika, lakini mimi nilikuwa naomba labda niulize. Je, ni kwanini Serikali pengine iingie sasa ubia? Kwa sababu iko haja kuwepo hata na hosteli wale wanaosubiria wagonjwa wanalala nje kabisa kwa sababu ya matatizo ya sehemu za kusubiria wagonjwa wetu? Ahsante (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, nimemuelewa. Anachokizungumzia ni kwamba Hospitali yao ya Mkoa wa Iringa iko kwenye eneo dogo na upande mwingine wapo Magereza, ambao kumekuwa na mjadala mkubwa. Kwamba wataka hospitali ile ihamishwe ipelekwe sehemu nyingine kwenye eneo ambalo ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, lakini investment iliyofanyika kwenye eneo lile ni kubwa sana kiasi kwamba ukihamisha harakaharaka utadororesha huduma za tiba. Sasa nimuombe Mheshimiwa Mbunge wakati Mkuu wa Mkoa na Wizara tukijadiliana kabla maamuzi hayo hayajafanyika atupe Subira, kwa sababu kuna mambo ya muhimu kwanza yanafikiriwa kati ya TAMISEMI lakini pia na sisi Wizara ya Afya na masuala yote ya tiba ili tuweze kufanya huo uamuzi.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.

Barabara ya Mahenge inayopita Udekwa inatokeza mpaka Ilula ni barabara muhimu sana, ni barabara mbadala ya barabara ya Mlima wa Kitonga kama magari yakikwama.

Je, ni lini Serikali itaipa umuhimu mkubwa sana ili barabra hii ijengwe kusiwepo na matatizo inapotokea katika barabra ya Kitonga, magari yaweze kupita katika hii barabra? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabra ya Mahenge mpaka kwenda Ilula kama barabara ya mchepuko tunatambua umuhimu wake na tutawatuma TARURA Mkoa wa Iringa waende wakafanye tathmini halisi na watuletee ili tutafute fedha kwa ajili ya utengenezaji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwanza nishukuru sana majibu ya Serikali, lakini sisi humu sote ndani wote ni watu wenye ulemavu watarajiwa na lazima tukiri kwamba mtu mwenye ulemavu hawezi kutoka point A kwenda point B kwa kutumia vyombo vya usafiri kwa sababu miundombinu haikidhi haja kabisa na katika jibu la Waziri amesema kwamba kuna TBS kuna LATRA ambao wanatakiwa kuangalia hivyo viwango;

Je, ni ipi sasa kauli ya Serikali kutoka na hili jambo ili watu wenye ulemavu na wenyewe wapatiwe haki ya msingi ya kupanda haya mabasi?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali langu la pili, watu wenye ulemavu wamekuwa wakinyanyapaliwa sana katika vituo vya mabasi na madaladala wakati wa kuingia katika hivi vyombo, kwa sababu kuna watu wasioona kuna watu ambao hawawezi kutembea unaona kwamba wanapata manyanyaso makubwa sana.

Je, ni utaratibu gani mzuri sasa ambao umewekwa kuhakikisha kwamba hawanyanyaswi na wanawekewa mpango mzuri wa kupanda katika hivi vyombo vya usafiri?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa balozi mwema wa watu wenye ulemavu. Kwa swali la kwanza anataka asikie kauli ya Serikali, kauli ya Serikali ni hii; kwanza natoa wito kwa wamiliki wote wa vyombo vya usafiri, daladala pamoja na mabasi na kwa kushirikiana na LATRA pamoja na TBS wahakikishe ya kwamba wanaweka miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuwanyanyapaa watu wenye ulemavu hususan katika maeneo ya stendi ama mabasi, hili tunatoa onyo kali sana kwa sababu watu wenye ulemavu ni binadamu kama binadamu mwingine yeyote na ahaki zote za msingi. Kwa maana hiyo, kupitia vyombo vyetu vya sheria na kupitia Jeshi la Polisi pamoja na TARURA pamoja na TANROADS kuhakikisha kwamba miundombinu yote wezeshi hususan barabara pamoja na mabasi kwa maana ya vyombo vya usafiri kwa wale wamiliki tunaweza kuhakikisha hivyo vinawekwa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nisisitize hapa suala la kisheria kwa mtu yeyote atakayeonewa, tutahakikisha tunachukua sheria kali sana na itakuwa fundisho kwa watu wengine wote wanaonyanyapaa na kuwanyasa watu wenye ulemavu.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kijiji kidogo cha Msukanzi katika kata ya IIlula kimerukwa kuwekewa umeme lakini kata inayofuata kuna umeme. Sasa ni lini Serikali itaona umuhimu kwamba kuruka hivi vijiji si kitu kizuri, ili vijiji vyote viwe vinapata umeme kuliko kuacha kimoja hafu vingine vinapata?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, Iringa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuhakikishie yeye pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba katika awamu hii ya tatu mzunguko wa pili ambayo ni ya mwisho hakuna kijiji kitakachoachwa. Tulipita humu Bungeni kwa Waheshimiwa Wabunge kuwaomba watuambie vijiji ambavyo vinadhani vimeachwa na tukavichukua tukaviweka kwenye orodha. Kwa hiyo kama kuna Mheshimiwa Mbunge yoyote anayedhani kuna kijiji ambacho kimerukwa kwa taarifa alizokuwa nazo basi tuwasiliane tukichukue kwa sababu sisi kwa taarifa tulivichukua vyote. Hata hivyo nitaenda pia kuwasiliana na Mheshimiwa Ritta Kabati, ili tukione hicho kijiji ambacho kimebaki tukichukue kama anavyosema.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la msingi.

Kwa kuwa shule nyingi sana za sekondari, za msingi na vyuo zina viwanja vibovu sana na Mheshimiwa Waziri amesema kwamba kuna baadhi ya halmashauri tayari zimeanza kutenga hizo fedha. Je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na jambo hilo kwa sababu watoto wetu wanakosa haki yao ya msingi ya kutengeneza vipaji vyao?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara na kama Serikali tulishatoa kauli kwamba katika shule zetu tuhakikishe tuna miundombinu ya michezo. Hivyo nitoe rai kwa halmashauri zetu, vyuo na maeneo ambako vijana wetu wanahitaji miundombinu hiyo waendelee kutenga, lakini wavitunze na waviendeleze.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Je, ni lini Mheshimiwa Waziri atakuja katika Mkoa wetu wa Iringa katika machimbo ya Nyakavangara, Kata ya Malengamakali, Jimbo la Ismani ili aje aone changamoto kubwa za wachimbaji wadogo wadogo pamoja na uwezeshaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, napenda kumjibu Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara ya Madini kupitia taasisi zetu za Tume ya Madini, GST na STAMICO tumeweka mkakati kabambe wa kuzungukia nchi nzima kuwajengea uwezo wachimbaji wadogo, kutatua kero zao na kuhakikisha kwamba wanafuata sheria, kanuni na taratibu katika kujipatia maeneo ya kuchimba madini. Hatukuishia hapo tumehakikisha kwamba katika maeneo yote yenye machimbo tunaanzisha masoko ya madini na vituo vya kununulia na kuuzia madini.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali madogo mawili. Kwanza nashukuru kwa majibu ya Serikali. Kilimo cha uhakika ni kilimo cha umwagiliaji. Napenda kufahamu hatua iliyofikiwa kwa utekelezaji wa miradi ya Mgombilenga iliyopo Kata ya Kitwiru na Mradi wa UNI wa Kata ya Nyanzwa, kwa sababu hii miradi, Wabunge wa Iringa ni muda mrefu sana tumekuwa tukiifuatilia.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, katika Wilaya ya Mufindi Kaskazini tuna skimu ya Igoma, Kata ya Sadani na Ikwea. Hii miradi kwa mfano hii ya Ikweha ililetewa shilingi milioni 800, lakini utekelezaji wake mpaka sasa hivi bado haujaweza kueleweka. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atujibu, Mkoa wetu wa Iringa ni wa kilimo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu miradi ya Mgombilenga na Nyanzwa iliyopo Wilaya ya Kilolo, katika bajeti ya mwaka 2022/2023 Serikali itakwenda kuikabarati miradi hii na kuitekeleza. Hivyo nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili la mradi wa Ikweha, ni kweli pale tuna mradi ambao mpaka hivi sasa umeshatumia shilingi milioni 800 ambazo zimetokana na fedha za DADPs pamoja na DIDF. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tunafahamu changamoto iliyoko pale, hivi sasa Serikali tunatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa bwawa. Vile vile mimi mwenyewe nitakwenda kutembelea mradi huu ili kutatua baadhi ya changamoto zilizopo pale na kuwafanya wakulima wawe na amani na kufanya kilimo cha umwangiliaji katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwahidi tu Mheshimiwa Mbunge, kama Serikali, tunafahamu changamoto iliyopo pale na tunatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa bwawa.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mikoa ya Iringa, Ruvuma, Njombe na Rukwa ilikuwa inajulikana kama The Big Four kwa kilimo cha mahindi, lakini wakulima wengi sasa hivi wametetereka sana kutokana na bei kubwa ya pembejeo.

Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba bei ya pembejeo inapungua ili mikoa hiyo iendelee kulima kilimo kikubwa kabisa cha mahindi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ambayo Serikali tutaichukua kumpunguzia maumivu ya pembejeo mkulima katika bajeti inayokuja tutaanzisha Mfuko maalum, (Price Stabilization Fund) ambao ikitokea pembejeo zitakwenda juu Serikali itatoa ruzuku ili mkulima asiumie sana katika upatikanaji wa pembejeo.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo ya nyongeza. Ninamshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa kuna vikundi ambavyo vimekuwa vikijishughulisha na utunzaji wa mazingira na yeye mwenyewe amekiri hata wanafunzi wameendelea kufungua program zao. Changamoto kubwa vikundi hivi vinakuwa vina ukosefu wa fedha ili viweze kufanya vizuri zaidi.

Je, Serikali inawasaidiaje, vikundi hivi viendelee kupanda miti mingi na kuendelea kutunza mazingira ambayo wanayaishi?

Swali la pili, ili kupunguza shughuli za kibinadamu kuzunguka milima na vyanzo vya maji.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwezesha kufanya shughuli zingine kama za ufugaji, uvuvi, katika maeneo ambayo wanazunguka wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS - MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa vikundi mbalimbali ambavyo vinahitaji kusaidiwa, lakini tunajiridhisha na kuangalia umuhimu wa vikundi hivyo na kwa kiasi gani wanasaidia na wao katika kuimarisha mazingira ndani ya milima lakini na vyanzo vya maji. Serikali ipo tayari kabisa kuwasaidia vikundi hivyo kwa ajili ya kuimarisha mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, namna gani tutawezesha, tutawezesha kwa kuwapatia taaluma mbalimbali na kuwaita katika mikutano yetu ili kuwapa taaluma kwa ajili ya kuimarisha mazingira ndani ya nchi yetu.
MHE: RITHA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, upembuzi yakinifu wa daraja hilo umeshafanyika na wananchi wa Nsimbo wanataka kujua. Je, katika bajeti hii daraja hilo litajengwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili. Barabara ya kutoka Kayenze mpaka Kaliua ni lini itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati ambayo ameuliza kwa niaba ya Mheshimiwa Anna Richard Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Nsimbo ambaye amekuwa anafuatilia sana ujenzi wa barabara hii. Daraja la Ugalla kama nilivyosema katika jibu la msingi lina urefu wa mita 150 lakini linaunganishwa na madaraja mengine saidizi makubwa zaidi ya matano na makalavati zaidi ya tisa makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi Serikali imeanza kuyajenga madaraja hayo saidizi ili tuweze kulifikia hilo daraja kubwa. Kwa hiyo, tayari Serikali imeshaanza kujenga hayo madaraja saidizi na makalavati. Kuhusu ujenzi kwa kiwango cha lami kuanzia eneo la Kawajenzi ambapo ni Mpanda Mjini kupita hilo Daraja la Ugalla hadi Kaliua ujenzi huo utaanza baada ya kukamilisha kuifungua hiyo barabara.

Mheshimiwa Spika, hii barabara ni barabara mpya ambayo inapita katika Mbuga ya Kaliua, upande wa Mkoa wa Katavi tumeshafungua mpaka kwenye daraja lakini upande wa Tabora kwa maana ya kutoka Ugala hadi Kaliua bado tunaendelea kuifungua. Kwa hiyo, baada ya kuifungua tutatafuta fedha kuijenga barabara hiyo sasa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Lini Serikali itatenga fedha za kutosha ili barabara inayotoka Mtandika kwenda Ikula iweze kujengwa kwa sababu barabara ile ni hatarishi sana na wakati wa mvua haipitiki wanawake wajawazito wanapandishwa mshikaki kwenda katika kituo cha afya kujifungua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii barabara ya kutoka Mtandika kwenda Igula na vijiji ambavyo amevitaja Mheshimiwa Mbunge ni kweli ni barabara muhimu na inapelekea wananchi kufika kwenye kituo cha afya kwa ajili ya huduma za afya. Kwa hivyo Serikali itaendelea kufanya tathmini ya gharama zinazohitajika ili fedha iweze kutafutwa na kuiboresha barabara hiyo ili kipindi cha masika iweze kupitika vizuri na wananchi waweze kupata huduma nzuri za usafiri, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Kata ya Kimala ipo pembezoni sana mwa Wilaya ya Kilolo na hakuna Kituo cha Afya, katika ile Kata barabara hazipitiki wananchi wanaenda katika Kituo cha Afya cha Dabaga.

Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuwajengea Kituo cha Afya katika Kata hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kata hii ya Kimala ambayo iko pembezoni tulishaelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo kufanya tathmini na kuwasilisha Kata za kipaumbele za kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa vituo cha afya. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Mkurugenzi kufanya hayo maelekezo ya Serikali na kutuletea, ikiwa ni kipaumbele cha Halmashauri hiyo basi Serikali itaona namna ya kutafuta fedha kushirikiana na mapato ya ndani lakini pia fedha za Serikali Kuu kwa ajili ya ujenzi. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo ya nyongeza. Kwa kuwa katika Hospitali ya Ocean Road kuna changamoto ya baadhi ya mashine za mionzi kukaa muda mrefu bandarani kutokana na kutokamilika kwa taratibu za kikodi; je, Serikali ina mpango gani wa kuweka utaratibu mzuri wa vifaa tiba hivyo kuondolewa mlolongo wa taratibu hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, Serikali sasa haioni haja ya kuondoa kodi zote kabisa ya vifaa tiba vyote vya wagonjwa wa kansa, figo na kadhalika ili hospitali nyingi ziweze kutibu hayo magonjwa na kutibu Watanzania walio wengi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu uliopo sasa ni mzuri, kwani Mheshimiwa Waziri wa Afya akisharidhia tu, basi vifaa hivyo vinapatiwa msamaha wa kodi.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi, ni kwamba vifaa tiba vyote vikiwa vya kansa, figo na kadhalika vinapatiwa msamaha wa kodi baada ya kupata ridhaa tu ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, ahsante.

SPIKA: Kwa hiyo, tutakuwa sahihi kwamba anayechelewesha vifaa ni Wizara ya Afya na siyo Wizara ya Fedha.

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, sisi tukipata tu barua ya Mheshimiwa Waziri wa Afya kuhusu vifaa tiba, basi tunatoa msamaha bila pingamizi yoyote.

SPIKA: Waziri wa Nchi, naona Waziri wa Afya hayupo wala Naibu wake. Huu ndiyo uhalisia? Kwa sababu haya maneno ya Mheshimiwa Mariam Kisangi, maana yake atakuwa kayatowa Ocean Road, wanasubiria vifaa viko bandarini.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, naomba suala hili tulichukue, tutalifanyia kazi vizuri Serikalini ili tuwe na majibu ambayo yana uhakika na tuweze kumkabidhi Mheshimiwa Mbunge na kuona tatizo hilo linaweza likahitimishwa namna gani. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini barabara ya kilometa tano ya kutoka Kinyanambo C – Mapanda mpaka Kisusa, Jimbo la Mufindi Kaskazini, itajengwa? Kwa sababu hii barabara inafungua uchumi wa Mufindi Kaskazini.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge Viti Maalum, Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii aliyoitaja ni kweli inafungua uchumi, lakini ujenzi wake pia utategemea na upatikanaji wa fedha. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kadiri fedha zitakavyokuwa zinapatikana, barabara hii itajengwa yote kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Vile vile nitoe masikitiko yangu makubwa sana kwa haya majibu aliyotoa, kwa sababu mchakato huu wa kuhamisha gereza ili hospitali iweze kufanya kazi vizuri siyo wa leo wala wa jana, ni wa muda mrefu sana; je, huu mchakato ni lini utakamilika? Kwa sababu haya majibu nimekuwa nikipatiwa muda mrefu, naomba leo anipe jibu, lakini siyo la mchakato tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili. Kwa niaba ya akina mama wa Mkoa wa Iringa naomba kumpongeza Daktari Bingwa wa Magonjwa ya akina mama, Dkt. Mwakalebela. Kwa kweli anawatendea haki akina mama, na vifo vya watoto vimepungua; lakini tunayo changamoto ya muda mrefu sana kwa Daktari Bigwa wa Upasuaji wa Mifupa. Wananchi wa Iringa wanapata ajali nyingi sana, hata jana kuna ajali pale Kitonga imetokea; hili tatizo tumeshalileta muda mrefu Serikali, lakini hatupatiwi Daktari, wananchi wanapata shida kuja Dodoma au kwenda Dar es Salaam: Je, ni lini sasa huyu Daktari Bingwa wa Upasuaji atakuja katika Mkoa wetu wa Iringa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa jinsi anavyofuatilia huduma za afya, siyo tu kwa Hospitali ya Mkoa wa Iringa, lakini kwa Wilaya zake za Mkoa wa Iringa kwa kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge wa Majimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ni mchakato utaisha lini? Namwomba Mheshimiwa Mbunge, mimi na yeye twende pamoja Wizarani na tutamwonyesha mchakato ulipofikia na tutaendelea kwa pamoja tuumalize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizungumzia Hospitali ya Mkoa, siyo suala la majengo tu, ni suala la skills zilizopo pale na teknolojia iliyosimikwa kwenye hospitali. Kwa hiyo, ni kazi. Ukisema uchomoe hiyo teknolojia haraka ukahamisha, utavuruga huduma za afya kwenye mkoa. Kwa hiyo, ndiyo maana mambo mengi yanachelewa pamoja na mawasiliano na Wizara ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu Daktari Bingwa wa Mifupa, kama alivyosema Mheshimiwa Waziri wa Afya, Bunge liliopita, kwa hospitali yetu ya Iringa kwa mchakato unaoendelea sasa hivi ndani ya Wizara kuhamisha madaktari, Iringa wanahitaji kupelekewa Daktari wa Mifupa, Daktari wa ENT na Daktari wa Neurologist. Kwa hiyo, tumelipokea na litafanyiwa kazi mara moja. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza: -

Je, Serikali inawasaidiaje kwa dharura wananchi wa Kata ya Ruaha Mbuyuni, Wilaya ya Kilolo kwa kuwa wameingia taharuki kubwa sana; mfereji umeacha njia, umehama, intake imeachwa peke yake, maji hayapo kabisa: Wananchi hawali, hawalali, maji hayapo kabisa na mashamba yamekauka?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli eneo la Ruaha Mbuyuni mfereji umehama na mto umehama. Kwa hiyo, hatua ambayo Serikali inachukuwa sasa hivi, timu ya Wataalam wa Wizara ya Kilimo tayari iko Mkoani Iringa kwa ajili ya kuliangalia hilo eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la msingi ambalo nilitaka nilitaarifu Bunge lako na wakulima wa eneo la Ruaha Mbuyuni, tatizo la Ruaha Mbuyuni halitofautiani na tatizo lililokuwepo kwenye maeneo ya Mlenge na Mkombozi. Kila mwaka mvua zikiwa nyingi mto huacha njia. Kwa hiyo, hatua tuliyoamua kama Wizara, tunaenda kulifanyia detailed design na kutangaza baadaye kwa mwaka ujao wa fedha ili ijengwe comprehensive scheme katika lile eneo na tuondokane na hili tatizo la kila mwaka kwenda kufanya repair katika eneo hilo. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa barabara yetu ya Kitonga kumekuwa na ajali nyingi sana, na wiki iliyopita tu basi lilitumbukia pale, na ajali ikitokea magari yanakaa takriban siku nzima au siku mbili. Je, lini Serikali itaona sasa umuhimu wa kujenga barabara mbadala ya kutoka Mahenge kwenda Udekwa kupitia Utalisoli mpaka Ilula?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika,ni kweli lile eneo la Kitonga limekuwa na changamoto kubwa. Tayari Serikali ilishatoa maelekezo kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa wasaidiane na Meneja wa TARURA Mkoa wa Iringa kuangalia uwezekano wa kufanya by-pass ya Mlima Kitonga ili kunapotokea changamoto kuwe na uwezekano wa kuwa na njia mbadala, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza je, ni lini mradi wa Mgambalenga katika kata ya Ruaha Mbuyuni utakamilika, kwa sababu toka mwaka 2014 umeanza kujengwa lakini haupatiwi pesa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika skimu 42 ambazo zilifanyiwa upembuzi yanikifu na usanifu wa kina katika mwaka wa fedha 2022/2023 ni pamoja na skimu ya Mgambalenga. Hivyo katika Mwaka 2023/2024 skimu hii itaendelea kufanyiwa ukarabati wa miundombinu na kazi itafanyika kwa uharaka zaidi ili wakulima waweze kupata fursa ya kufanya kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, lakini nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake japokuwa hali ni mbaya sana wakati wa mvua katika lile eneo naomba wajitahidi kufanya haraka sana.

Naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza; kwa kuwa barabara ya Kinyanambo C - Mapanda mpaka Ukami na Kinyanambwa A Saadani – Igoma katika Jimbo la Mufindi Kaskazini ni ya kiuchumi na pia ni ya ahadi ya Mheshimiwa Rais; je, ni lini itajengwa kwa kiwango cha lami?

Swali la pili, barabara ya Iringa – Kilolo - Idete ni ya mkoa na Serikali iliahidi muda mrefu sana kuiunganisha na mkoa wa Morogoro kupitia kata ya Idete, Itonya, Muhanga mpaka Mungeta; je, ni lini ahadi hiyo itatimia kwa sababu uchumi wa mkoa wa Morogoro na Iringa uweze kukua kwa urahisi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Dkt. Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia suala hili la barabara ya Kinyanambo C-Mapanda mpaka Ukome. Ni ahadi ya viongozi wetu wa kitaifa na ahadi zote za viongozi wa kitaifa sisi Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi tutahakikisha tunazitekeleza na tunaziweka katika vipaumbele vya bajeti ya mwaka 2023/2024, hususani kwenye barabara hii ya Kinyanambo C -Mapanda-Ukoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, barabara hii ya Iringa – Kilolo – Idete kipande cha Ipogolo – Kilolo chenye kilomita 33 ni barabara ambayo inafadhiriwa na Benki ya Dunia na mwaka huu wa fedha tunaoendelea nao, wapo katika hatua za manunuzi na kilometa 67 zilizobaki nazo zimekwishafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Kwa hiyo, niwahakikishie wananchi wa maeneo haya kwa sababu unaunganisha kati ya Mkoa wa Iringa pamoja na Morogoro kwamba inakwenda kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafsi niulize swali dogo la nyongeza. Huu ugonjwa wa figo, ugonjwa ambao unatesa sana, kuanzia sasa hivi mpaka watoto wadogo sana; lakini gharama za matibabu ni kubwa sana. Wakati sasa hivi bima haijaanza kwa nini wasiondoe gharama kwa ugonjwa huu tu, Kwa sababu watu wengi wanakufa kwa sababu ya kukosa pesa ya matibabu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mlisikia juzi kwenye bajeti yetu kwamba Rais wetu ametoa bilioni tano kwa ajili ya kuwasaidia watu wasiojiweza kwenye eneo hili la matatizo ya figo na mengine. Lakini bado tuna utaratibu mzuri sana kama nchi wa kuweza kuwapa exemption wale ambao hawajiwezi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nafikiri kikubwa ambacho naendelea kukuomba Mheshimiwa Mbunge uwe balozi mzuri wa bima ya afya kwa wote kwa sababu ni suluhisho la kudumu kwenye matatizo haya. Tuna magonjwa mengine hapa ni asilimia 15, hii ni asilimia saba, wanateseka sana watanzania. Kwa hiyo mimi ninachosema tuwe mabaloozi wazuiri wa bima ya afya kwa wote tutapata suluhisho la kudumu kwenye tatizo hili.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Iringa ni kati ya Mikoa iliyohamasisha kulima kwa wingi zao la parachichi, changamoto inayowakabili ni bei kubwa sana ya miche ya mbegu. Je, ni lini Serikali itaona umuhimu hata kuwapatia miche ya ruzuku ili wananchi waweze kulima kwa wingi zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu ya Awamu ya Sita kama nilivyosema, chini ya Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeongeza fedha nyingi sana kwenye sekta hii ya kilimo na ninyi ni mashahidi kutoka billioni 200 mpaka karibu trilioni moja sasa. Moja ya maeneo ambayo yameangaliwa ni kuongeza ruzuku kwenye uzalishaji wa miche ya mazao mbalimbali ikiwemo parachichi. Hii tayari tumeshaweka na kule Iringa tayari pale Kilolo kuna miche ambayo inazalishwa kwa ajili ya ruzuku.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni muda tu kwamba wakulima wawasiliane na Idara ya Kilimo katika Mkoa wa Iringa ili waweze kupata miche ya ruzuku kwa ajili ya kupanda zao hili la parachichi. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kitonga ni barabara ambayo ni ya Kitaifa na imekuwa ikipitisha malori makubwa, inapopata ajali kidogo malori yamekuwa yakikwama kwa siku nzima au siku mbili, Serikali ilikuwa imetuahidi kujenga barabara mbadala ambayo itatokea Mahenge – Kudekwa kupita Wotalisoli mpaka Ilula.
Je, ni lini sasa ile ahadi ya Serikali itatekelezeka ili kuondoa changamoto kubwa katika Mlima Kitonga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tuna kazi mbili ambazo tunazifanya, moja ni kuendelea kuipanua ile barabara ili iwe pana hasa hilo eneo la Kitonga, kuruhusu magari yaweze kupishana na kunapotokea changamoto tupate nafasi ya magari mengine kupita.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni kweli Serikali ina mpango wa kujenga bypass (njia ya mchepuko) kuchepusha kupita huo Mlima Kitonga kunapotokea changamoto na tumeunganisha nguvu kati ya TANROADS na TARURA ambao wanaendelea na usanifu wa hiyo barabara, baada ya hapo hiyo barabara itajengwa, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu gani unafanyika kuwapeleka Madaktari Bingwa kama wakiwa wamehamishwa, kwa sababu Mkoa wetu wa Iringa sasa ni karibu mwaka wa tatu Daktari Bingwa wa Mifupa amehamishwa na hatujampata na kuna ajali nyingi sana. Je, ni lini sasa tutampata katika hospitali ya Mkoa wa Iringa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nalichikua tatizo lake kama alivyolisema kuona tunalishughulikiaje, lakini jana Mheshimiwa Waziri wa Afya ameelekeza Idara ya Utumishi wakishirikiana na Idara yetu ta IT na kuwasiliana na Utumishi ili tuwe tunaweza kuona kwenye mfumo jinsi ambavyo watumishi wa afya wamegawanyika maeneo mbalimbali na hiyo itaturahisishia kuona ni namna gani, maeneo gani ambayo yana upungufu, ni maeneo gani wamezidi watumishi kwa namna hiyo tutakuwa tunapanga kwa kujua vizuri wamezidi wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nakubaliana na wewe kwamba Madaktari Bingwa wengi wako Dar es Salaam, wako kwenye Miji mikubwa na Waziri ameshatoa maelekezo kuona namna gani iyo Mikoa ya mbali wanapelekwa hao Madaktari Bingwa. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, Je, ni lini Serikali itajenga minara ya simu Kata ya Mapanda na Kibengu katika Jimbo la Mufindi - Kaskazini kwa sababu wananchi wanapata shida sana ya mawasiliano? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, maeneo ya Kibengu hayapo katika minara 758 lakini tunayaingiza kwenye tathmini ya minara kwenye vijiji 2,116. Kwa hiyo, tukishakamilisha na fedha zikapatikana, tutafikisha mawasiliano katika Kata hiyo, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa changamoto kubwa ya wakulima wetu nchini ni upatikanaji wa mbegu bora; je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba mbegu bora zinapatikana kwa wakati ukiwemo Mkoa wangu wa Iringa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mkakati wa Serikali kwa kutumia Wakala wa Mbegu Tanzania (ASA) na wazalishaji binafsi kuhakikisha tunazo mbegu za kutosha kuweza kuwahudumia wakulima wa nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya mbegu za kilimo katika mpango wetu ule wa Agenda kumi thelathini ifikapo mwaka 2030 ni kuwa na uzalishaji wa tani takriban laki sita na Hamsini elfu. Hivi sasa tupo katika uzalishaji wa tani 61,000 kama asilimia kumi ya mahitaji yetu katika mwaka 2030.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge, hivi sasa kwenye mashamba yetu yote ya ASA tumeweka mifumo maalum ya umwagiliaji ambayo itatuhakikishia uzalishaji wa mbegu zaidi ya mara mbili ndani ya mwaka mmoja, na hivyo wakulima wetu watapata mbegu kwa wakati kwa sababu hivi sasa tumeboresha mashamba yetu 16 na mbegu zitaanza kuzalishwa zaidi ya mara moja ndani ya msimu.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Je, ni lini wananchi wa Kata ya Ng’ang’ange katika Wilaya ya Kilolo watapatiwa fedha ya mradi wa maji au kuchimibwa visima ili waweze kupata majisafi na salama kwa sababu sasa hivi wanatumia maji ya mito? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakupongeza Mheshimiwa Dkt. Ritta, hata juzi nimekuona ukiwa na Mheshimiwa Waziri Aweso kuhakikisha changamoto ya maji inakwenda kutatuliwa ukiongozana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo. Vile vile katika kata hii uliyoitaja ya Ng’ang’ange sisi kama Wizara tunafahamu na tunakwenda kupeleka utatuzi kwa kuchimba visima na unafahamu gari tumeshaifikisha, umeiona wewe mwenyewe. Kwa hiyo, kisima hiki kitachimbwa ndani ya mwaka ujao wa fedha. (Makofi)

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa muda wa kuuliza maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, huu mradi umechukua muda mrefu sana kwenye utekelezaji wake, na Serikali tayari ilikuwa imeshaweka zaidi ya shilingi milioni 800 katika mradi huu. Wananchi wa Mufindi Kaskazini wameusubiri kwa muda mrefu sana. Je, Serikali sasa katika bajeti hii iko tayari kufanya huo upembuzi yakinifu na kuanza ujenzi wa mradi huu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, utekelezaji wa maagizo ya Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Comrade Chongolo alipotembelea Mradi wa Umwagiliaji wa Ruaha Mbuyuni katika Wilaya ya Kilolo kwa sababu ulikuwa una changamoto kubwa sana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la kwanza; ni kweli zmetumika shilingi milioni 800 katika hatua ya awali ambayo kazi yake kubwa ilikuwa ni ujenzi wa banio, njia ndefu ya kilometa 3.5 pamoja na vivuko, lakini katika Mwaka wa Fedha unaokuja tumetenga fedha kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, ili kupata chanzo cha uhakika cha maji katika skimu hii, ili iweze kufanya shughuli za umwagiliaji mwaka mzima.

Mheshimiwa Spika, jambo hili pia, tulikaa na Mbunge wa jimbo, Mheshimiwa Kigahe, tulizungumza kwa pamoja namna ya kuweza kuboresha skimu hii na hasa katika kuhakikisha kwamba, tunajenga bwawa hilo kwa ajili ya chanzo cha maji cha uhakika.

Mheshimiwa Spika, la pili la kuhusu Ruaha Mbuyuni; tulipokea maelekezo ya Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi na tayari mimi na Mheshimiwa Aweso tulishatuna timu ya wataalamu kwa ajili ya kwenda kuangalia, kufanya marejeo ya usanifu wa eneo lile na hasa kurudisha Mto Lukosi katika njia yake ya asili, ili iweze kusaidia maji yale yaende katika mashamba ya wananchi na yasilete athari. Na hivi sasa kazi inaendelea, naamini baada ya muda mfupi ujao tutapata gharama halisi na utekelezaji utaanza mara moja.

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Serikali itawajengea askari polisi wa Wilaya ya Kilolo kwa sababu hawajawahi kujengewa nyumba, wanaishi kwenye nyumba za kupanga? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeanza kutoa maibu yangu kwamba, tutahakikisha katika bajeti ambayo tumeeleza hapa katika jibu letu la msingi, tutahakikisha kwamba tunaanza ama tunaendeleza kujenga nyumba za makazi, kwa sababu kama tulivyosema mwanzo hiyo changamoto tunaifahamu na tunajua kwamba askari wetu wengi wanaishi kwenye nyumba nyingi zimechakaa, lakini tutahakikisha kwamba tunawajengea nyumba na makazi ya kisasa ili waweze kukaa kwenye makazi mazuri na kuweza kutoa huduma vizuri kwa wananchi.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa Wilaya ya Kilolo imekuwa na changamoto nyingi sana na katika Wilaya hiyo hiyo kuna Kata ya Mahenge, Ukwega, Lugalo na Ihimbo wananchi wanapata shida sana ya mawasiliano.

Je, ni lini sasa Serikali itaondoa changamoto hizo ili wananchi wa Kilolo waweze kupata mawasiliano ya uhakika?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Iringa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Kilolo walileta maeneo takribani 12 ambayo yalikuwa na changamoto ya mawasiliano, lakini eneo la Ilambo, Itimbo, Lugalo, Udekwa, Ukwega tayari tumeweka minara ya mawasiliano na huduma zinaendela.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kata nyingine ambazo tumezipelekea fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo takribani shilingi bilioni 1.28 imekwishapelekwa kwa ajili ya kujenga minara nane katika Kata saba za Jimbo la Kilolo, nakushukuru sana.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafsi niulize swali la nyongeza. Je, lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Ilula, Ibumu ili ijengwe japo kwa kiwango cha changarawe tu na madaraja manne ili wananchi waweze kupita, manake sasa hivi wanapata mateso makubwa sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakaa na Mheshimiwa Kabati kuona kama barabara hii ya Ilula - Igumu imewekwa katika mradi wa Agri-connect ambao wao Iringa ni wanufaika wa mradi huu. Kama haijawekwa basi kuona ni namna gani bajeti ya TARURA ya Wilaya ya Kilolo inaweza ika-accommodate barabara hii katika mwaka wa fedha unaofuata na kama sio mwaka wa fedha unaofuata basi ule wa 2024/2025.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafsi niulize swali la nyongeza. Je, lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Ilula, Ibumu ili ijengwe japo kwa kiwango cha changarawe tu na madaraja manne ili wananchi waweze kupita, manake sasa hivi wanapata mateso makubwa sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakaa na Mheshimiwa Kabati kuona kama barabara hii ya Ilula - Igumu imewekwa katika mradi wa Agri-connect ambao wao Iringa ni wanufaika wa mradi huu. Kama haijawekwa basi kuona ni namna gani bajeti ya TARURA ya Wilaya ya Kilolo inaweza ika-accommodate barabara hii katika mwaka wa fedha unaofuata na kama sio mwaka wa fedha unaofuata basi ule wa 2024/2025.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Kwanza kabisa niipongeze Serikali kwa kuona watoto wengi wamerudi mashuleni, lakini mimi swali langu nilitaka kuuliza; je, Serikali inatoa elimu ya makuzi na malezi kwa hawa watoto ili hili tatizo lisiweze kujitokeza tena katika watoto wengine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunatoa elimu hiyo ya makuzi na malezi, lakini nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge katika rasimu ya mitaala pamoja na sera ambayo tunaendelea nayo hivi sasa, maoni ya wadau mbalimbali yameonesha kwamba kuna uhitaji wa masomo haya ya makuzi na malezi. Kwa hiyo, katika mitaala ijayo mambo haya tunaweza kuyaona kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.

Ni kwa nini sasa Serikali inapoita vijana kwa ajili ya usaili isiangalie hizo sifa na vigezo kuliko hivi sasa pengine nafasi ni ishirini wanaitwa watoto 3,000 mpaka 5,000? Wanasababisha vijana wengi kuteseka hapa Dodoma wakati wa kusubiri huo usaili. (Makofi)

Swali langu la pili, ni kwa nini vijana wengi wamekuwa wakijitolea au kupewa nafasi za mikataba lakini inapotokea ajira hawa vijana hawapati kipaumbele, wamekuwa wakijitolea miaka minne, mitano kiasi kwamba zikitoka ajira wanaajiriwa wapya. Hii kwa kweli inaumiza sana na inaliza sana kwa vijana wetu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali maswali mawili ya Mheshimiwa Ritta Kabati kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na nafasi chache wanaitwa wengi, katika maelezo ya msingi nilieleza kwamba nafasi za ajira kwa sasa kwa mujibu wa kanuni ambazo zimepitishwa na Bunge lako ni nafasi za kiushindani. Hivyo tunapotangaza matangazo matarajio yetu ni kwamba watajitokeza wengi ili waje kushindana kwa ajili ya kupata nafasi hizo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli nakiri mbele ya Bunge lako kwamba malalamiko juu ya wingi wa wanaoomba na dhidi ya nafasi kuwa chache umeendelea kujitokeza. Serikali yako imeendelea kufanya juhudi za dhati kuhakikisha kwamba tunakabiliana na changamoto hii. Lakini kupitia Bunge lako maelekezo yalishatolewa na Ofisi ya Rais inayoshughulikia Utumishi imeyachukua na inakwenda kuyafanyia kazi na tutapokuwa tayari tutaleta majibu mbele ya Bunge lako.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili kuhusu wale wanaojitolea halafu baadaye wanakuja kukosa ajira. Wakati naeleza katika swali la msingi, ajira za Serikali zinazingatia sifa, taaluma, uwazi na usawa, na ni maelekezo ya Bunge lako kwamba katika uwazi huo na usawa huo, ulielekeza kwamba ajira zinapotolewa waitwe watu wadahiliwe kwa usawa na uwazi, sasa inapotokea kwamba mtu aliyepo kazini anakosa kazi hili tena linakuwa niseme ni jambo la kiufundi zaidi na siyo jambo la mtu kuonewa. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wanaofanya kazi waendelee kuhakikisha kwamba wanashindana vizuri ili waendelee kupata kazi kama ambavyo wengine wamekuja kwenye ushindani.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Barabara ya Kalenga – Wasa - Mafinga ni barabara muhimu sana kwa uchumi katika Mkoa wetu wa Iringa. Je, katika kilometa 100 za Mradi wa RISE kwa nini wasipatiwe japo kilometa 10 tu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Barabara ya Itimbo – Kitelewasi inapita katika milima na miteremko mikali, hivyo inahitaji kujengewa makalavati. Je, Serikali ipo tayari sasa kujenga makalavati ili wananchi wa Kitelewasi na Itimbo waweze kupita kwa uraisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Sika, ahsante sana. Kwanza natambua kwamba kuna mahitaji makubwa ya ujenzi wa barabara hususani katika maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameainisha. Barabara ya Kalenga mpaka Mafinga ambayo ina urefu wa kilometa 100 hususani hizi za RISE na amekuwa akiomba kilometa kumi, niseme tu kwamba zile barabara zimeshawekwa katika mpango wake. Kwa hiyo kikubwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI itazingatia katika mipango ijayo ili kuona sasa tunatafuta hizo kilometa 10 waweze kujenga katika maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyataja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Barabara ya Itimbo – Kitelewasi ambayo ina mteremko mkali, mahitaji ya Kalavati, nafikiri kwa kutumia fedha za Mfuko wa Dharura, Ofisi ya TARURA Mkoa wa Iringa tuwaelekeze tu kwamba kulingana na mahitaji ya maeneo hayo, waipe kipaumbele barabara hii, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika taarifa yao ya Wizara ya Kilimo walisema sasa hivi wakulima watakuwa wanapimiwa udongo kupitia Maafisa Ugani kwa vishkwambi. Elimu hiyo sasa wakulima wanayo maana yake nimeona bado hawajaanza kutumia hiyo teknolojia ya kupimiwa udongo katika mashamba yao?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ni mkakati wa Serikali kuhakikisha tunapima afya ya udongo ya ikolojia zote saba nchi nzima ili wakulima wawe na taarifa sahihi za afya ya udongo katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa Serikali kupitia Maafisa Ugani tumewapatia scanners za kwenda kupima afya ya udongo ambayo itasaidia kutoa taarifa kwa wakulima. Vilevile katika mwaka wa fedha unaokuja tutakwenda kununua mobile lab ambazo zitakuwa pia zinapita kwa ajili ya kuwapimia afya ya udongo wakulima. Kwa hiyo, tutakuwa tunao uwezo wa kupima afya ya udongo kupitia maabara na kupitia katika magari pamoja na kit ambacho tumewapa Maafisa Ugani ambapo mkulima akipimiwa afya yake ya udongo hapo hapo akiwa shambani atapata cheti chake ambacho kitaonesha katika udongo huo kuna nutrients za aina gani na anahitaji nini kupanda zao gani na atumie mbolea ya namna gani, ambayo itakuwa ni ukombozi mkubwa kwa wakulima wa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa, katika Mji wa Ilula uliyoko katika Wilaya ya Kilolo unao mradi ambao umeshakamilika kwa muda mrefu lakini changamoto kubwa ni usambazaji wa maji katika vitongoji vyote.

Je, lini Serikali au katika bajeti hii itatoa pesa ili maji yaweze kusambazwa katika Mji wa Ilula? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabati kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe ni shahidi Mheshimiwa Kabati ni mfuatiliaji mzuri sana wa miradi ya maji kukamilika. Suala la mradi ambao tayari umekamilika usambazaji unafuata hiyo ndiyo hasa Wizara inashughulika nayo. Sisi tunapenda kusema mradi umekamilika pale maji yanapotoka bombani mwananchi ananufaika. Hivyo kwa mradi kama huu ambao umekamilika usambazaji ndiyo hatua inayofuata kwa mwaka ujao wa fedha.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Je, Serikali itamaliza lini uwanja wetu wa ndege wa Iringa, kwa sababu uwanja ule tunategemea sasa hivi Mama amehamasisha royal tour kwa ajili ya utalii mkubwa katika hkivutio cha Ruaha na vivutio vingine vilivyoko katika Mkoa wa Iringa na Nyanda za Juu Kusini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba ujenzi huu unaendelea. Serikali inaendelea kuujenga uwanja huu na Wakandarasi wako site. Pengine tu ni kuwahimiza Wakandarasi waweze kuongeza speed na tunajenga kwa fedha ya Serikali pia wenzetu wa World Bank wameonesha utayari wa kuweza kusaidia ili kukamilisha ujenzi wa uwanja huu ili kuweza kuimarisha shughuli za utalii ambazo tayari Mheshimiwa Rais ameshakuwa champion wa hiyo kazi. Kwa hiyo tunakuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba uwanja huu tutaukamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Ni lini Serikali itafungua zahanati katika Kijiji cha Pomelini Kata ya Ng’uruhe Jimbo la Kilolo kwa sababu wananchi walichangia na Serikali imeshamalizia kile kituo kwa muda mrefu; na wananchi wanakuwa wakifuata matibabu umbali mrefu sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge, kwa swali hili ambalo ameliuliza nitamwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kilolo pamoja na DMO waende wakafanye tathmini ili watuletee ili ifanyiwe usajili na ili tuweze kuifungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia ametangaza kwa nguvu kubwa utalii kupitia Royal Tour na kwa kuwa barabara zinazokwenda katika Mbuga za Wanyama kama Ruaha National Park hadi leo hazijajengwa kwa kiwango cha lami.

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara zote zinazokwenda katika mbuga za wanyama zinajengwa kwa kiwango cha lami ili watalii watakapokuja tutendewe haki na Nyanda za Juu Kusini tupate watalii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa kuanza na barabara ya Iringa kwenda Ruaha National Park, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami barabara hiyo, lakini pia Benki ya Dunia (World Bank) imeonesha nia ya kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa maana ya barabara zote zinazoenda kwenye mbuga kama ukipitia kwenye kitabu chetu cha bajeti barabara nyingi zinazokwenda kwenye mbuga zimefikiriwa na kutengewa fedha ili kuboresha sekta hii ya utalii ambayo Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan tumeona jinsi ambavyo amefanya kwenye Royal Tour kwa hiyo na sisi hatutamwangusha kuhakikisha kwamba tunatengeneza miundombinu bora kwa ajili ya watalii kwenda kwenye mbunga za wanyama, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri na naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tarehe 8 Agosti huwa ni siku ya wakulima nchini, na siku hiyo wakulima wengi hupata fursa ya kukutana kuonesha maonesho na kujifunza, na kwa kuwa Serikali imesimamisha haya maonesho karibu mwaka mmoja na nusu sasa.

Je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na kusimamishwa Maonesho haya ya Nanenane nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa kuwa kumekuwa na vikwazo vingi sana barabarani kwa magari yanayosafirisha bidhaa hizi za mazao yanayoharibika kama nyanya, parachichi na kadhalika na kusababisha hasara kubwa sana kwa wakulima.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutoa vibali maalum kwa ajili ya magari yanayosafirisha mazao haya kwa saa 24, kwa sababu kuna magari makubwa ambayo yanazuiwa, saa 12 yanaambiwa yasisafirishe mazao kupeleka hata nje ya nchi kama South Africa? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, zao la parachichi na mfumo mzima wa parachichi katika nchi yetu haukuwa na mwongozo. Kwa hiyo Serikali sasa hivi iko kwenye hatua za mwisho na tutazindua mwongozo wa kusimamia zao la parachichi kuanzia shambani mpaka sokoni na utaratibu wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kupitia Bunge lako tukufu wakati tunafanya mawasiliano ndani ya Serikali kati ya Wizara ya Kilimo, TRA na watu wa TANROADS kwa maana ya Wizara ya Miundombinu ili ku-develop stika maalum ambazo zitasimamia mazao ya horticulture, magari yote yanayobeba mazao ya horticulture yatakuwa na stika maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka nipitie Bunge lako tukufu kuziomba Mamlaka za Serikali za Mitaa kwamba mazao ya parachichi na mazao ya mbogamboga ni perishable, ni vizuri kutokuweka vikwazo visivyokuwa na ulazima barabarani kwa kipindi hiki ambacho tunaandaa mwongozo ambao utasimamiwa ndani ya Serikali katika ngazi zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo huu utaratibu wa kuwazuia kusafiri usiku nadhani siyo sahihi na ninapenda kupitia Bunge lako tukufu kuwaomba viongozi wa mikoa wa-facilitate transportation ya mazao ya kilimo hata kama ni usiku namna gani. Kama mtu anasafiri aendelee na kusafirisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kipengele cha pili kuhusu Nanenane; ni kweli Serikali ilisimamisha Nanenane kwa muda, na ninataka kupitia Bunge lako tukufu kuwatangazia Watanzania na wakulima kwamba Nanenane tunarudisha na mwaka huu Kitaifa itafanyika Mkoa wa Mbeya. Serikali iko kwenye kufanya total reform ya mfumo wa Nanenane. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ningepitia Bunge lako tukufu kuzitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa; shughuli za Nanenane zitasimamiwa na Wizara ya Kilimo na sekretarieti za mikoa. Taasisi iliyokuwa inaitwa TASO ambayo ilikuwa imejimilikisha kusimamia Nanenane haitahusika na wala haihusiki na masuala ya Nanenane na viwanja vya Nanenane. Suala hili litasimamiwa na Serikali, Wizara ya Kilimo na Mamlaka za Mikoa kwa maana ya mikoa husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali sasa hivi tuko kwenye hatua za mwisho za kuandaa mfumo mpya wa shughuli za Nanenane, na Tanzania tutakuwa na kitu tunaitwa Tanzania International Agricultural Trade Show ambapo tutakuwa na eneo moja ambalo nchi nzima kila mwaka kimataifa litakuwa linafanyika hapo na mikoa itakuwa inafanya shughuli za kikanda. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa barabara inayopitiwa na Mlima Kitonga ni barabara ambayo imekuwa ikipata ajali nyingi na imekuwa ikipitisha mpaka wagonjwa wanaopelekwa hospitali ya Muhimbili.

Je, Serikali sasa iko tayari kujenga kwa kiwango cha lami barabara mbadala ili kama magari yakichelewa kupita pale kwa siku mbili au siku tatu; barabara ya Mahenge - Udekwa inayokwenda kutokezea Ilula ili wananchi waweze kupita kama magari yamekwamwa muda mrefu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge, kwanza kumpongeza kwa kutoa hilo wazo na sisi kama Serikali tumelichukua ili kweli kwamba kunapotokea changamoto basi tuwe na alternative ya kuweza kupitisha hasa kama kutatokea suala la wagonjwa kama alivyosema. Ahsante.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa sasa hivi kuna malalamiko mengi sana kwa baadhi ya wanafunzi wanufaika wa hii mikopo ya vyuo vikuu wamekuwa wakimaliza madeni yao lakini bado mfumo unaendelea kukata madeni yao.

Je, Serikali inasemaje kuhusiana na hawa wanafunzi ambao bado wanaendelea kukatwa wakati wameshamaliza madeni?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Kabati kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niweze kumpongeza Mheshimiwa Kabati kwa ufuatiliaji wa karibu wa jambo hili nadhani ameshakuja ofisini si chini ya mara moja/mara mbili kwa ajili ya kufuatilia jambo hili.

Mheshimiwa Kabati kwanza nikuondoe wasiwasi, sasa hivi utaratibu wetu kila mnufaika wa mikopo ile ana akaunti yake na katika akaunti ile inakuwa inaonyesha kwamba kiasi gani amelipa na kiasi gani kilichobaki kwamba hajalipa. Kwa mantiki hiyo iwapo kama kuna wanufaika ambao wanaendelea kukatwa wakati wameshamaliza ile mikopo, tuna dawati letu la malalamiko la kuonesha kwamba yeye amekamilisha, lakini bado anaendelea kulipwa au anaendelea kukatwa kwenye mishahara au kwenye mafao yake mengine.

Kwa hiyo, hili suala tunaendelea kulifanyia kwa sababu ni suala la kimfumo, lakini nikuondoe wasiwasi wale wote ambao wamekatwa kwa namna moja au nyingine tumekuwa tukizirudisha fedha hizi baada tu ya kuleta hayo malalamiko ili kuweza kuwarudishia wao wenyewe. Nakushukuru.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Mkoa wetu wa Iringa kuna msitu Mufindi, Mgololo na kuna msitu katika Wilaya ya Kilolo na moto kila wakati umekuwa ukitokea katika hiyo misitu; ni lini Serikali itaona umuhimu wa Wilaya ya Kilolo na Wilaya ya Mufindi kupatiwa gari la zimamoto?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Ritta Kabati swali lake la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba maeneo ya Mufindi na Mgololo mara kadhaa hukumbwa na majanga ya moto, niombe tu uongozi wa zimamoto Mkoa wa Iringa waweze kupangilia vizuri rasilimali za magari walizonazo ili angalau gari moja liwe kwenye Wilaya ya Mufindi kuwa na ukaribu kwenye maeneo ambayo majanga hutokea zaidi. Nashukuru.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Mkoa wetu wa Iringa kuna stendi ile ya Igumbilo tunashukuru, lakini stendi ile iko mbali sana na wananchi imekuwa ni mateso wananchi wamekuwa wakifika usiku sana wanapigwa na wajambazi.

Je, hivi ni kanuni au sheria kwamba haya mabasi yasishushe abiria katika stendii za zamani kwa sababu wananchi wengi wengi wanapata mateso makubwa sana?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali siku zote ni kuboresha huduma za wananchi, lakini pia kurahisisha Maisha ya wananchi katika maeneo yao. Kwa hiyo naagiza Mkuu wa Mkoa wa Iringa lakini na menejimenti nzima ya Mkoa wa Iringa kufanya tathimini ya athari ambazo zinatokana na kuacha kutumia stendi ya zamani na kutumia stendi mpya peke yake na kuona busara inaongoza nini ili wananchi wapunguziwe adha ya usafiri. Ahsante sana.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Barabara ya Mgololo - Mafinga itajengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu hii barabara ni kitega uchumi katika Jimbo la Mufindi Kusini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara ya Mgololo – Mafinga ni kati ya barabara sita ama saba ambazo tunazijenga kwa utaratibu wa EPC + F na nimelijibu mara kadhaa kwamba tayari kazi zinaendelea za awali kwa wakandarasi ambao wamepatikana kuijenga hii barabara. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ni kati ya barabara ambazo zinatekelezwa kwa Mpango wa EPC + F na tutahakikisha kwamba hiyo barabara inajengwa kama Serikali ilivyoahidi, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa, Mheshimiwa Naibu Waziri alipotembelea Machimbo ya Nyakabangala katika Jimbo la Isimani, aliwaahidi kuwaleta watafiti na kuwapatia vifaa ili wananchi waweze kuchimba kwa uhakika zaidi.

Je, ni lini sasa ile ahadi itatimia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, hivi sasa tumeanza kuwatawanya sana wataalam wetu kupita maeneo tofauti tofauti ya nchi, na lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunawaongoza wachimbaji waweze kuchimba katika kanuni na taratibu za kisheria pasipo kubahatisha. Kwa hivi sasa tumeanza kusambaza pia mitambo yetu ya uchorongaji ambayo itawasaidia wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kanda ya Mikoa ya Iringa, Njombe pamoja na Mkoa wa Mbeya tayari tuna mtambo ambao uko kule. Tutatoa maelekezo kwamba uwafikie pia na wachimbaji wa eneo hilo ambalo Mheshimiwa Mbunge amelisema ili nao waweze kupata huduma. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali mawili. Kwa kuwa Chuo hiki tayari kina technical na academics staff zaidi ya 231 wakiwemo zaidi ya Maprofesa 70. Pia huduma mbalimbali toshelezi wapo mpaka wanafunzi wenye mahitaji maalum. Ni kwanini sasa Serikali isitoe kibali chuo hiki kijitegemee na muda maalum wa uwangalizi wa vigezo hivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Rais wetu alipokuja katika Mkoa wa Iringa alipoongea na Wazee aliahidi kutoa fedha kupitia Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu kwa ajili ya ujenzi wa majengo mbalimbali ya chuo.

Je, ni lini sasa Serikali itatimiza ile ahadi ya Mheshimiwa Rais kwa sababu hiki Chuo kinatakiwa kiwe fanisi katika Nyanda za Juu Kusini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika ni kweli Chuo chetu kina Watumishia hao aliowataja Mheshimiwa Mbunge zaidi ya 231 wakiwepo Maprofesa hao 70 lakini kwa vigezo hivi siyo vigezo pekee ambavyo vinatumika kwa ajili ya kupandisha hadhi chuo hiki na naomba nimpe taarifa tu Mheshimiwa Mbunge, Maprofesa hawa waliopo wengi wao ni wale ambao wameazimwa kutoka katika Chuo Mama kile Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Kipekee wale ambao walioajiriwa na Chuo Kikuu cha Mkwawa pale kwa upande wa Maprofesa hatuna hata Profesa mmoja ambaye ameajiriwa kama Mwajiriwa wa chuo kile pale.

Mheshimiwa Spika, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwanza tumebeba ushauri wake, lakini naomba nimuhakikishie Serikali hivi sasa tumepata Mradi wa HEET ambao unakwenda kusomesha Maprofesa na Maprofesa wasaidizi zaidi ya 100 ambao tutahakikisha sasa baada ya mafunzo yao hawa, chuo hiki kinaweza kupandishwa hadhi kuwa Chuo Kikuu kinacho jitegemea.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la pili la upande wa majengo. Tumshukuru sana Mheshimiwa Rais lakini tumshukuru vilevile Waziri wa Fedha kwa upande wa mapato yetu ya ndani mwaka uliopita wa fedha na mwaka huu wa fedha tumeweza kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi pale wa majengo na mpaka hivi ninavyozungumza Wakandarasi wawili wako pale site ambae ni SUMA JKT pamoja na Salimu Construction. Salimu Construction anafanya ujenzi pale wa hostel na SUMA JKT wanafanya ujenzi wa library.

Mheshimiwa Spika, vilevile katika Mradi wetu wa HEET tumeishapeleka pale jumla ya dola za kimarekani milioni nane kwa ajili ya kuongeza miundombinu pamoja na majengo mbalimbali kukifanya Chuo kile kiwe na hadhi ya kupandishwa kuwa Chuo Kikuu kamili, nakushukuru.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa, Mheshimiwa Naibu Waziri alipotembelea Machimbo ya Nyakabangala katika Jimbo la Isimani, aliwaahidi kuwaleta watafiti na kuwapatia vifaa ili wananchi waweze kuchimba kwa uhakika zaidi.

Je, ni lini sasa ile ahadi itatimia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, hivi sasa tumeanza kuwatawanya sana wataalam wetu kupita maeneo tofauti tofauti ya nchi, na lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunawaongoza wachimbaji waweze kuchimba katika kanuni na taratibu za kisheria pasipo kubahatisha. Kwa hivi sasa tumeanza kusambaza pia mitambo yetu ya uchorongaji ambayo itawasaidia wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kanda ya Mikoa ya Iringa, Njombe pamoja na Mkoa wa Mbeya tayari tuna mtambo ambao uko kule. Tutatoa maelekezo kwamba uwafikie pia na wachimbaji wa eneo hilo ambalo Mheshimiwa Mbunge amelisema ili nao waweze kupata huduma. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Je, ni lini Wilaya ya Kilolo itajengewa ofisi ya Makao Makuu ya Polisi kwa sababu ni muda karibu miaka 20 haijajengewa Makao yalipo Makuu ya Wilaya?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jibu la swali hili linafanana na jibu ambalo nilijibu katika swali la mwanzo juu ya mikakati na jitihada za Serikali za kutatua changamoto za vituo vya Polisi katika ngazi mbalimbali ikiwemo Wilaya ya Kilolo. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge avute subira wakati jitihada hizo zikiwa zinaendelea.(Makofi)