Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Asha Mshimba Jecha (13 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa ufanyaji kazi ya utumbuaji majipu na nchi yetu kuwa ni mahali salama na wananchi wetu kukabiliana na maisha yao bila ya vikwazo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu kwa kazi nzuri anazozifanya. Naamini kwa muda mfupi ujao maendeleo ya wananchi wetu yataboreka. Aidha, nawapongeza Mawaziri na Manaibu Mawaziri kwa utendaji kazi kwa kuwa karibu na wananchi, kubaini changamoto zinazowakabili na kuzipatia ufumbuzi wa haraka.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hoja hii ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Watanzania wameridhika na juhudi zinazoendelea kuchukuliwa katika kuwabaini wafanyakazi hewa na kuchukuliwa hatua zinazostahili. Kundi hili ni kubwa lina mtandao mrefu na usiri wa hali ya juu, lakini kila mmoja akichukua wajibu wake vita hii tutashinda.
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kazi wanazofanya kuangalia na kusimamia maadili ya Viongozi wa Umma. Nashauri Tume hii kuangalia na njia nyingine kwa kuwafikia wananchi ambao siyo Viongozi wa Umma katika utaratibu unaoeleweka, lakini wamekuwa viongozi katika mfumo usio rasmi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi nzuri inayofanyika, nakubaliana na Wizara kuona ipo haja kufanya utafiti kwa waajiri na wadau mbalimbali ili kubaini changamoto ambazo zimekuwa zinalalamikiwa mfano, baadhi yao walipofuatilia Utumishi walijibiwa na mhusika kwamba bado haja-prove na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mfuko wa Kujitegemea (PTF) ni wa muda mrefu na umeweza kuwafikia watu wengi hasa wanawake. Tunashauri Mfuko huu utangazwe zaidi ili wananchi wetu waweze kufaidika nao.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Naipongeza Wizara hii kupitia Waziri, Naibu na Watendaji wote kwa kazi ngumu mnayokabiliana nayo katika Wizara hii, kwani kazi ya kusimamia na kuiendeleza taaluma kwa kiwango cha ubora ina changamoto nyingi, lakini penye nia pana njia, msivunjike moyo tuko pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimba kwa wanafunzi wa kike. Umefikia wakati sasa kwa wanafunzi wa kike wanaopata mimba baada ya kujifungua waruhusiwe kuendelea na masomo kama kuna Sheria kandamizi ziletwe Bungeni tuzibadilishe.
Bodi ya Mikopo. Pamoja na jitihada kubwa za Serikali kuwapatia mikopo baadhi ya wanafunzi wanaostahili, lakini kumekuwa na changamoto na kama Wizara/Bodi ya Mikopo haikuzifanyia uchunguzi maalum, basi ile dhana ya kuwapa mikopo wanaostahili haitafikiwa kwa usahihi na mikopo iliyoiva kushindwa kurejeshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migomo na maandamano kwa wanafunzi/wanavyuo. Kero ya maandamano na migomo kwa wanafunzi inazorotesha elimu kwani huharibu mazingira na vifaa na wakati mwingine husababisha maafa na hasara kubwa na hata shule kufungwa na wanafunzi kukosa masomo na kurudi majumbani. Wizara ina mkakati gani wa kuzuia changamoto ya maandamano na migomo, hasa kwa yale ambayo yamo ndani ya uwezo wao kwani tumeshuhudia baadhi ya wakati mara tu wanapogoma au kuandamana, kile wanafunzi wanacholalamikia Wizara inawapatia haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Dira na Dhima ya Wizara ni nzuri na kama tutaitafsiri kwa vitendo na kuwashirikisha wadau mbalimbali na kila mmoja wetu akitimiza wajibu wake hakuna lisilowezekana. Hivyo, tunaiomba Wizara iandae mipango mikakati ya muda wa kati na muda mrefu ili kubaini ushiriki mpana na wa wazi katika kufikia Dira ya Wizara ya Elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Elimu ya Juu ni suala la Muungano, hivyo pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Wizara kwa kushirikiana na upande wa Zanzibar (Wizara ya Elimu), ipo haja sasa kukaa pamoja wadau wa elimu wa pande hizi mbili za Muungano ili kubaini changamoto na kuzitafutia njia muafaka za utatuzi, hasa ukizingatia tumo katika mchakato wa ushirikiano wa Afrika Mashariki na nchi yetu pia, inakabiliwa na utandawazi. Ni muhimu tujiandae sasa, wakati hautusubiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuendeleza maliasili zetu na watalii wanaoingia nchini mwetu wanaongezeka siku hadi siku. Ni jambo jema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kama tutajipanga vizuri kwa kuutangaza utalii na vivutio tulivyonavyo, mapato yetu yanayotokana na utalii yataongezeka zaidi. Mfano, utalii wa viungo; tuwahamasishe wananchi wetu kupitia mtu mmoja mmoja au vikundi kuanzisha mashamba ya viungo (spices) mbalimbali na watalii wataona kitu kingine badala ya wanyama pekee na wananchi wataongeza vipato vyao moja kwa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali kuwaandaa wananchi kuvutia watalii kwa utamaduni wetu wa asili, mfano ngoma zetu za asili, mila na desturi zetu za asili, mavazi, chakula, lugha, malezi na kadhalika. Kwa utalii wa historia utahusu watawala waliopita na kutawala.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. ASHA M. JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Naipongeza Wizara kupitia Mheshimiwa Waziri, Naibu, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote kwa juhudi kubwa wanazofanya kushughulika na afya za Watanzania na kuboresha maendeleo ya jamii. Sambamba na hilo ni weledi wao ulioifanya Wizara hii kusonga mbele na kuleta mabadiliko makubwa ya kiutendaji na kuwahudumia Watanzania popote walipo mjini na vijijini. Hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezeshaji wanawake kiuchumi. Naipongeza Wizara kwa mipango mizuri ya kuwainua wanawake kiuchumi. Hata hivyo, bado juhudi zaidi zinatakiwa kuchukuliwa kwani bado wapo wanawake wengi wajasiriamali hawajawezeshwa kiuchumi, wanajitahidi wenyewe lakini kutokana na mtaji kuwa mdogo wanashindwa kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Benki ya wanawake, iko mbali na wanawake walioko vijijini. Je, ni lini Wizara itaielekeza benki hiyo kufungua angalau dirisha katika maeneo ya vijijini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hisa katika Benki ya Wanawake, wapo baadhi ya Wabunge tumeshiriki kununua hisa kwa ajili ya uanzishwaji wa benki hii. Je, ni lini tutaarifiwa juu ya kinachoendelea na hatma yetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuongelea kuhusu unyanyasaji wa wanawake na watoto. Naipongeza Serikali kwa juhudi mbalimbali inazochukua katika kukabiliana na tatizo hili lakini bado juhudi zaidi zinahitajika kwa kuungana pamoja kupiga vita hali hii isiendelee. Wazee/wazazi waache tabia ya kuwatumia watoto wadogo kama kitega uchumi kwa kuwaingiza katika ajira za watoto hasa kuwatumikisha majumbani na kuwakosesha haki zao za elimu na matunzo ya karibu ya wazazi. Kwa nini Wizara isielekeze ajira za majumbani zifanywe na watu wazima badala ya kuwatumia watoto wadogo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa uamuzi wake wa kuitangaza elimu kuwa bure na tumeshuhudia wingi wa wanafunzi wakitumia fursa hiyo. Mwenyenzi Mungu atakulipa kwa upendo wako kwa Watanzania na kujali utu na kutoa haki ya elimu kwa wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ongezeko la wanafunzi mashuleni limekuwa kubwa, nashauri Wizara kuwa na programu maalum ya ajira kwa walimu kwa mkataba kwa kuwatumia walimu wastaafu kwa muda mfupi na wa kati, ili kujiandaa na ajira mpya kwa wale walimu watakaomaliza mafunzo, kuwezesha kuziba pengo la ukosefu wa walimu kutokana na wingi wa wanafunzi.

Kuhusu ujauzito kwa wanafunzi wa kike, tunaiomba Wizara kukamilisha mchakato wa sheria ya kuendelea na masomo kwa wanafunzi wanaopata mimba mara tu akishajifungua. Utafiti unaonesha kwamba wale waliopata mimba mara baada ya kujifungua, wakakubali kurudi shule kwa hiari wamefanya vizuri katika masomo yao na wamefaulu na kuendelea na masomo ya juu. Mifano hiyo ya wanafunzi hao iko Zanzibar ambapo tayari tumepitisha sheria ya watoto wa kike wapatapo mimba shuleni kurudi shule mara baada ya kujifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo elimu zaidi itolewe kwa wanafunzi wote kujitambua kutokana na mabadiliko ya miili yao ili wawe na ufahamu wa jinsi ya kujilinda na unyanyasaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi sahihi ya lugha ya kiswahili, je, Wizara ina mipango gani wa lugha ya kiswahili kuikuza na kuzungumzwa kwa usahihi hasa ukizingatia kuwa lugha hii sasa inazungumzwa na nchi nyingi za Afrika na Tanzania ndiyo lugha yetu. Hadi sasa Tanzania imetoa wataalam wangapi wa lugha ya kiswahili kufundisha nje ya nchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii.
Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Naipongeza Wizara kupitia wanajeshi wetu kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuilinda nchi yetu na kubaki katika hali ya utulivu na amani. Hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vijana wanaojiunga na JKT mara wamalizapo mafunzo ya kujitolea (kujitegemea), baadhi yao huajiriwa na vikosi vyetu vya ulinzi, lakini baadhi hurudi katika maeneo yetu na kuzurura bila kazi maalum ya kufanya. Je, Serikali haioni sasa wakati umefika kwa vijana hawa wanaopitia JKT kuwa na mfuko maalum wa kuwasaidia vijana hawa mara tu wamalizapo mafunzo, kupewa na kuanzisha miradi na kujiajiri wenyewe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wakati wakiwa JKT wapewe mafunzo ya ujasiriamali ili wakitoka wawe tayari kujiajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Maji ni uhai, kila chenye uhai kinahitaji maji. Hivyo napongeza juhudi kubwa inayochukuliwa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kupitia Wizara hii kwa jitihada ya kuwafikishia huduma hii wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mahitaji ya maji ni makubwa katika nchi yetu na tunashuhudia wakati huu wa mvua za masika maji mengi yanavyopotea, tunaiomba Wizara ya Maji iandae program mahususi ya kuvuna maji ya mvua ambayo kwa sasa yanapotea bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango mwingine ni kuwaelimisha wananchi au taasisi, mfano shule, vituo vya afya na kadhalika, wavune maji kupitia mapaa ya nyumba na kuyahifadhi. Kwa wafugaji wenye mifugo mingi waelimishwe kujiandalia mazingira yatayowezesha kuhifadhi maji hasa wakati wa mvua ambapo maji mengi hupotea bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, akinamama kwa asilimia kubwa ndio wanaosumbuka na watoto wao kutafuta maji. Nashauri kuvitumia vikundi vya akinamama katika program mbalimbali za kuvuna maji na kuyahifadhi kwa matumizi endelevu. Tutumie na vikundi vya vijana kubuni njia nafuu za kuvuna maji kwa matumizi ya kilimo na mifugo katika kipindi hiki cha mvua, kwani maeneo mengi mvua zimefika kwa wingi na maji yanapotea bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii kwa kuongezea tozo kwenye mafuta ili kuongeza Mfuko wa Maji.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri aliyoiwasilisha kuhusu mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya fedha za ofisi yake na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2018/2019. Wanachama wa CCM tumeridhika nayo kwani imelenga nchi yetu kutoka katika uchumi mdogo na kwenda uchumi wa kati wenye kaulimbiu ya Tanzania ya Viwanda inawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushiriki wa wananchi katika kukuza uchumi nashauri Mikoa, Wilaya, Kata, Vijiji na Vitongoji viwe na uratibu unaoeleweka kwa wananchi na uwe wa wazi ili mwananchi azione fursa na kumrahisishia ushiriki wake kwa shughuli na miradi wanayoifanya. Fursa zilizopo zilenge kuwafikia na kuwashirikisha wananchi wa jinsi na rika zote mfano, vijana wa elimu ya juu, wanawake na wanaume mjini na vijijini pamoja na walemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wenye elimu ya kawaida wasiobahatika kupata elimu mijini na vijijini, wanawake, wanaume na walemavu nao wanao mchango mkubwa kwani kufeli shule si kufeli maisha. Mwelekeo wa kuwafikia kiurahisi ni kuwa na vikundi, ushirika, SACCOS, VICOBA na kadhalika. Elimu ya ujasiriamali kwa shughuli na miradi wanayopanga kufanya ni muhimu sana kupatiwa kabla na wakiendelea kwenye utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fursa za masoko ndani na nje ya nchi zisimamiwe kikamilifu na kupunguza au kuondosha urasimu usio na lazima ili kuwapa moyo na kuthamini kazi wanazozifanya, kuwakutanisha na taasisi za fedha na mabenki kuweza kukopa na kuongeza mtaji kwa gharama nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais Magufuli kwa kuwawezesha watoto wote wenye uwezo wa kuingia shule waruhusiwe bila ya malipo. Hali hii wananchi wameipokea na kuwapeleka watoto kwa wingi. Wananchi hasa wanyonge wameitumia kikamilifu fursa hii na watoto wengi walioshindwa kujiunga na shule kwa kukosa malipo sasa wameingia shule. Changamoto iliyopo ni uhaba wa majengo na Walimu. Hata hivyo naamini Serikali kupitia wadau mbalimbali na taasisi wanaungana pamoja kulipatia ufumbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukosefu wa vyuo vya VETA kwa kujifunza kazi za amali (kujitegemea) kwa vijana wengi ambao wameshindwa kuendelea na masomo ya juu. Ukosefu wa takwimu sahihi kwa vijana wanaomaliza vyuo ama elimu ya juu na fani zao walizosomea. Nashauri mikoa, wilaya tuanzishe utaratibu wa kuwatambua wasomi wetu na fani zao walizozihitimu ili iwe rahisi kuwatumia na kuwashajihisha kujiwekea pamoja na kutafuta fursa na kuzitumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kuzaliwa Tanzania unazidi kuimarika, wananchi wake wanaishi bila bugudha yoyote ili mradi havunji sheria. Kwa kuwa Muungano huu ni wa watu bila shaka zinaweza kuwepo changamoto za hapa na pale, lakini zisigeuzwe na wapinzani wetu kuwa chachu ya kuvunja Muungano wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Muungano wetu ni wa damu, hivyo changamoto chache zilizobaki tuzitafutie ufumbuzi ili uzidi kuimarika. Hotuba, mijadala, makongamano yaeleze kwa uwazi mafanikio makubwa yaliyopatikana ndani ya miaka 54 ya Muungano wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unyanyasaji wa wanawake na watoto. Pamoja na jitihada kubwa inayochukuliwa na Serikali yetu ya kuweka sheria na kuridhia mikataba ya Kimataifa kupiga vita unyanyasaji wa aina zote wa wanawake na watoto, mafanikio yameanza kuonekana. Wanawake wanaweza kujitetea na kudai haki zao na kufikiwa na fursa mbalimbali bila ubaguzi, tunapongeza na kushukuru. Kwa watoto kumezuka makundi maovu yanawabaka na kuwalawiti watoto wa kike/kiume, sheria kali zichukuliwe dhidi ya wahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia leo kusimama hapa katika Ukumbi wako huu wa Bunge, pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri na kubwa anayoifanya, tunaiona na mwenye macho haambiwi tazama. Pia nimpongeze Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tunamwona na yeye anavyoshiriki katika kuleta maendeleo ya Tanzania yetu. Niwapongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu, Waziri wa Afya, Naibu Waziri wa Afya pamoja na Watendaji wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnafanya kazi nzuri, Tanzania ni kubwa changamoto haziwezi zikaisha kwa siku moja, Wizara ya Afya ilivyokuwa jana siyo ya leo na tunavyoendelea itazidi kubadilika hatua baada ya hatua, c chapeni kazi Mwenyezi Mungu atawalipa kwa wema wenu mnaoufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia kuhusu Bima ya Afya. Tanzania bima ya afya kwa wote inawezekana, Mheshimiwa Waziri naomba tukae na taasisi mbalimbali na vikundi mbalimbali kuona jinsi gani wananchi wanaweza kujiunga na bima ya afya. Wananchi wengi wakiweza kujiunga na Bima ya Afya itaweza kupunguza matatizo mengi ya kiafya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyozungumza Mheshimiwa Azza asubuhi hapa, akasema kwamba sasa hivi inaelekezwa kwenye vikundi mjiweke pamoja, lakini kuna watu hawana vikundi kweli ila pesa wanazo, naamini watu wengi wakijitokeza kujiunga mmoja mmoja Wizara wanaweza mkakaa au taasisi zinaweza zikakaa zikawakusanya ule wingi wa vikundi ambao wanautaka. Kwa hivyo, mwananchi asikose bima ya afya kwa sababu hana kikundi cha kujiunga pamoja na kupata ile fursa ambayo wanavikundi wanaweza wakaipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusiana na afya ya uzazi, kwa kweli mwanamke anastahili kuenziwa, kutunzwa, kukingwa na unyanyasaji wowote ambao anaweza akaupata, kwa sababu bila ya mwanamke dunia hii isingeweza kuendelea. Kuna matatizo mengi ambayo yanamkumba mwanamke tumeona katika kitabu chako

Mheshimiwa Waziri umezungumzia tezi ya shingo ya kizazi lakini mwanamke wakati huo huo anakumbwa na fistula yote yanamkosesha raha mwanamke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suluhisho la hili wamesema wanzangumkwamba huduma hii isogezwe karibu na wananchi. Huduma kuifuata Dar es Salaam na sehemu nyingine kwenye hospitali za Kanda wananchi Tanzania hii wanaishi mbali sana na huduma wasipoipata kwa kweli uhai wao uko matatani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugonjwa huu wa saratani ya mlango wa kizazi siyo tatizo la muda mfupi linachukua muda mrefu linahitaji uwe na hela, kama huna hela huwezi kufuatilia huduma hii na unakuta watu wengine wanashindwa kupata huduma hii, kutokana na ukosefu wa hela. Tunaomba Mheshimiwa Waziri pamoja na juhudi Serikali yetu inayochukua lakini tuzidi kuangalia, kuokoa vifo ambavyo umezungumza humu kwamba asilimia kubwa akinamama wanakufa kutokana na saratani ya shingo ya kizazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie unyanyasaji wa watoto, Mheshimiwa Najma Giga amezungumza, kwa kweli watoto wananyanyasika sana. Mheshimiwa Waziri pamoja na juhudi tuliyochukua tumeridhia maazimio kanuni, matamko, sheria ya kumlinda mtoto bado tunawaona watoto wananyanyasika. Basi katika mikoa yetu tuanzishe sehemu maalum ya watoto hawa kuweza kuwasaidia, unawakuta watoto pamoja na kwamba tunasema wana wazee wao, wanahangaika mitaanim wanazurura mitaani, watoto wale wanasaidiwa saa ngapi, wakiugua wanatibiwa na nani na tunaona saa nyingine mtoto anafika mpaka kwenye vyombo vya habari anatangaza au anatangaziwa kusaidiwa ugonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli imefikia mahali katika mikoa yetu kuwe na sehemu ambazo wale watoto kama wameshindwa kutibiwa na wanahitaji kusaidiwa basi usaidizi wao uwe wa karibu, tusiende mpaka kwenye vyombo vya habari kutangaza ugonjwa kwa kweli ile hatumtendei haki yule mtoto ambaye anahitaji tumsaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo naomba nichangie katika Wizara hii ni uzazi salama kwa mama. Mheshimiwa Waziri pamoja na jitihada kubwa iliyochukuliwa na Serikali yetu lakini bado tuendelee kuokoa maisha ya mama na mtoto. Akinamama wengi wanapoteza maisha wakati wa kujifungua au wakati wa ujauzito, pengine inawezekana ni lile tatizo la asili la ukosefu wa lishe bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, ipo haja ya kuwatumia Maafisa wa Afya au Maafisa wa Maendeleo ya Jamii kuihamasisha jamii juu ya lishe bora ili wakati wa kujifungua basi akinamama waweze kujifungua salama na kupunguza gharama kubwa ambayo anaweza akaitumia wakati ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mimi sina zaidi isipokuwa naendelea kuipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi. Kwa kweli tumeona maendeleo makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia katika kudumisha Muungano wetu, basi siyo vibaya kuwa tuna mashirikiano ya karibu sana na upande wa Zanzibar kwa sababu Wizara ya Afya najua siyo Wizara ya Muungano, lakini magonjwa hayana mipaka na utaalam hauna mipaka, kwa hivyo siyo vibaya kuongeza ushirikiano wetu wa karibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa asilimia 100. Naipongeza Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kuhakikisha amani, usalama wa nchi yetu unaendelea kuimarika na wananchi wake kuishi bila ya hofu na kuendelea na harakati za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Makamanda na Wanajeshi wetu wote kwa kutekeleza majukumu yao ya ulinzi wa nchi yetu kwa weledi na ufanisi mkubwa na jeshi letu kutuletea sifa kubwa ndani na nje ya nchi. Hongera sana na Mungu atawalipa kwa uzalendo wao wa kujitoa muhanga kwa ulinzi wa nchi yetu, hakika kazi yao imetukuka na tunaithamini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, kuendelea kuliimarisha Jeshi letu hatua kwa hatua na wakati wote jeshi letu limeweza kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, hata pale zinapotokea baadhi ya changamoto, halikushindwa kukabiliana na changamoto hiyo na tuliweza kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, udhibiti wa sare za jeshi, hivi karibuni kumejitokeza matumizi ya sare za kijeshi na hata za polisi kutumika kwa kufanyia uhalifu na kujipatia fedha kwa njia isiyo ya halali. Hivyo, tunaomba Wizara kuwa makini na jambo hili, kwani inaonesha baadhi yao huziiba nguo hizi wakati wakiwa kazini na mara wanapostaafu na maisha kuwa duni, huanza kujihusisha na uhalifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wanaojiunga na Jeshi la Kujenga Taifa, wakimaliza mafunzo yao, baadhi yao huajiriwa kwenye Taasisi mbalimbali, lakini wapo wanaobaki mitaani mwetu. Naomba Serikali kupitia Wizara hii kuwatambua vijana hao pamoja na wale wanajeshi wastaafu katika mikoa, wilaya zetu ili kuwa na takwimu zao kwa lengo la kuwatumia pale wanapohitajika, hata kuanzisha vikundi vya uzalishaji na ulinzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.

Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi kuchangia katika Wizara hii. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia leo kusimama hapa tukiwa katika hali ya uzima na afya. Pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo wanafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ni Wizara ambayo ina maisha ya wananchi moja kwa moja kwa sababu inalinda raia lakini inalinda na mali zao. Kwa hivyo hapo utaona ugumu wa kazi hii wewe unayelindwa una mali, anayekulinda hana mali. Kwa hiyo, hii Wizara kwa kweli ina kazi ngumu . (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais. Katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri tumeona kuna mambo mazuri ambayo yameelekezwa kwa Jeshi letu la Polisi. Tunaomba mambo hayo yafanyike kwa utaratibu kama yalivyopangwa. Mheshimiwa Waziri nimshukuru mwaka jana katika mchango wangu nilizungumzia Kituo cha Polisi Dunga na nimepata habari kwamba tayari ujenzi umeanza. Kwa hiyo namshukuru na nampongeza Mheshimiwa Waziri na naomba fedha zipelekwe kwa wakati ili ujenzi uweze kuendelea vizuri na kile kituo kimalizike kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika Mkoa wangu wa Kusini Unguja tuna upungufu mkubwa wa magari kwa ajili ya kufuatilia shughuli mbalimbali za maaskari. Mkoa wetu una vituo vingi lakini kuna ukanda mkubwa wa utalii, hatuna magari, baadhi yamekuwa yakitumika magari yetu kuwasaidia askari ni wajibu wetu. Kwa hiyo, tunaomba katika haya magari ambayo nimeyaona katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri, basi na Mkoa wetu wa Kusini wasisahau kutuletea magari hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vie nimeona kuna ujenzi wa nyumba za maaskari, Mkoa wa Kusini na kuna baadhi ya vituo vinahitaji kusaidiwa nyumba za askari, kwa hivyo nayo wasitusahau pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka nizungumzie, nataka nisifu Wizara hii, kazi ya kulinda raia na mali zao ni kazi kubwa. Kwa hivyo, bado namwomba Mheshimiwa Waziri, elimu ya kutii sheria bila shuruti iendelee kutolewa kwa wananchi wetu, kwa sababu maelezo yanayoelezwa humu ndani inaonesha wazi kwamba bado wananchi wanataka kupata elimu ya kutii sheria bila shuruti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi na raia ni ndugu, ni kama watoto pacha sisi tunawategemea lakini kwa kweli kumekuwa na manung’uniko mengi ambayo mengine hayana ukweli, mengine yanaweza yakawa yana ukweli fulani, kwa hiyo, ipo haja ya elimu kutolewa kwa raia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nilipongeze Jeshi la Polisi, Zanzibar kulikuwa na wakati mgumu sana, lakini tunashukuru Jeshi la Polisi waliweza kuzuia ugumu ule na sasa tunaishi kwa amani na utulivu. Wizara wanafanya kazi nzuri lakini kwa kuwa kuna wahalifu wengine hawataki kuona uzuri huu, tunaomba kila mtu achukue nafasi yake sisi raia tuna nafasi ya kushirikiana na Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo na sisi tushirikiane nao na wao wanayo nafasi ya kushirikiana na sisi na wao washirikiane na sisi vizuri. Jeshi hili lisiwe na uadui kwa raia na sisi raia tusiwe na uadui kwa Jeshi la Polisi kwa sababu tukilikosa kwa kweli hatuwezi kuishi hata kidogo, tunauona umuhimu wa Jeshi la Polisi pale yanapotokea matatizo, lakini tumekuwa tunawalaumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia kitabu cha Mheshimiwa Waziri, pia wako askari walikufa katika kutekeleza majukumu yao na wengine waliuawa kama walivyouawa raia wengine, halifurahishi kwa sababu uhai wa mwanadamu hauna thamani ya kitu chochote. Hata hivyo, haya mambo yaende sambasamba, sisi raia tuweze kutii bila shuruti, nao askari baadhi yao kwa sababu na wao ni binadamu kama sisi na wao bila shaka wengine wana upungufu, yule mtu mmoja asiharibu Jeshi zima la Polisi ambalo linafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, waendelee na kazi nzuri, yale madogo madogo ambayo yanalalamikiwa tuyafanyie uchunguzi na tuyachukulie hatua. Kuna askari wanafanya kazi nzuri na wamekuwa wakidai posho zao muda mrefu. Mheshimiwa Waziri amefanya ziara Zanzibar na Mheshimiwa Naibu wake amefanya ziara, lakini hata Wakuu wa vikosi nao wamefanya ziara na wamekuwa wakiwaahidi, kwa hiyo tuwatimizie yale matakwa yao ambayo bado hawajafanikiwa .

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kidogo inaleta huzuni kwa sababu ninapoona mwenzangu tumeingia kazini wote mwaka 2013/2014, wao wamepata zile posho, wengine hawajapata, kwa kweli haileti picha nzuri na wako hawa wanaopata posho ya kazi maalum. Kuna wengine wamepata, lakini wengine hawajapata na wote wameanza kazi pamoja, wameingia kazini pamoja, wamefuatilia, wamekwenda mpaka Makao Makuu, lakini majibu hakuna. Kwa hivyo tuwatazame hawa watu, yale manung’uniko madogo madogo tuweze kuyaondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna baadhi ya askari wa FFU Machui, walishiriki katika ile Operesheni Tokomeza na wao pia wanasema hawakupata posho zao mpaka sasa hivi. Mambo mazuri mengi wanayafanya, lakini haya madogo madogo najua yako ndani ya uwezo wao, kwa hivyo tujitahidi na wao tuwakamilishie ili mambo yaweze kwenda vizuri, lakini kiujumla Jeshi la Polisi wanafanya kazi nzuri. Kazi mnayoifanya tunaiona, tusingeweza kuishi kwa amani na utulivu kama hawapo, kuwepo kwao kuna umuhimu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, yale niliyozungumza kuhusu vituo vya polisi wayatekeleze. Naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Magufuli katika utekelezaji wa Ilani ya CCM ya kuwaletea wananchi maendeleo kwa kasi na ufanisi mkubwa. Awamu hii tumeona miradi mikubwa inayofanywa kwa fedha zetu za ndani na kwa muda mfupi. Naamini uthubutu wa Mheshimiwa wetu, Watanzania tukiacha kufanya kazi kwa mazoea, tukiungana na mwendo kasi wa Rais wetu, muda mfupi ujao Tanzania itakuwa ya kupigiwa mfano kwa mageuzi ya kiuchumi na maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuamua kukifanya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Kihinga Mkoani Kigoma kuwa Kituo cha Utafiti wa Mbegu Bora za Chikichi. Ushauri wangu kwa Serikali, kupitia kituo chetu hiki kuangaliwe uwezekano wa kufanya utafiti kwa zao la tende kwa Mkoa wa Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la tende Dodoma, kwa mitende iliyopo inazaa vizuri sana na tende kiafya zina lishe nzuri. Hivyo, ni chakula kizuri kinacholiwa Tanzania kutoka nchi za Kiarabu. Kiufupi mitende Dodoma inazaa vizuri kuliko hata huko nchi za Kiarabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiujumla utafiti wa mazao mbalimbali unahitajika ili kuondokana na kilimo cha mazoea tulichokirithi kwa wazee wetu ili mazao yetu yawe bora na kuweza kuuza nje ya nchi na kutuingizia fedha za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali kwa hatua za makusudi za kunyanyua mchezo wa soka katika nchi yetu na tumeshuhudia timu zikifanya vizuri ndani na nje ya nchi, pamoja na mchezo wa ngumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na soka, pia tuna michezo mingi ambayo ikiangaliwa ipasavyo na kupewa msukumo nayo inaweza ikaitangaza nchi yetu na kuiletea faida kubwa. Hivyo ni vyema Serikali kupitia Wizara ya Michezo kukaa na vilabu vya michezo mbalimbali kuona mipango yao ili kuweza kuandaa mikakati ya kunyanyua michezo hiyo, mfano, netball, riadha, basketball, volleyball na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali kwa maandalizi ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika mwaka 2020. Sambamba na hilo, nashauri upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa vya Mtanzania, kwani vijana wengi waliotimiza umri wa miaka 18 bado wanahangaikia vitambulisho. Hivyo hawajapatiwa na bila ya kitambulisho huwezo kuandikishwa kwenye Daftari la Wapigakura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha majengo ya vituo vya Polisi na nyumba za makazi kwa Askari wetu. Naomba Serikali kutukamilishia ujenzi wa Kituo cha Polisi Dunga ambacho kinahitaji kiasi cha shilingi milioni 50 kwa matengenezo ya ndani; kuweka sakafu, madirisha, milango, plasta ya ndani na nje, hard board na uzio.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Polisi Makunduchi, nyumba za makazi ya Askari wa kawaida hali zake ni mbaya sana, mbovu. Tunaomba majengo hayo yajengwe upya.

Mheshimiwa Spika, naomba Maaskari wetu wapatiwe posho na stahili zao kwa wakati. Wapo Askari wameziomba posho hizo kwa kuandika barua, na katika ziara ya Mheshimiwa Waziri na Naibu pia, Askari wameziwasilisha changamoto hizo lakini hakuna hatua yoyote ya mabadiliko na hawajapatiwa hadi leo. Mbaya zaidi kuna Askari wameajiriwa mwisho kuliko wengine, tayari wamepatiwa posho hizi. Mfano, mwaka 2004 hawajapata posho lakini 2006 anapatiwa posho, wakati kazi yao ni moja, vyeo sawa na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, wapo Watanzania wengi hawajapatiwa Vitambulisho vya Taifa na wanashindwa kujitafutia fursa na kuzitumia kwa wakati stahiki. Basi tunaomba vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi vitumike katika kuzifikia fursa hizo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Ahsante.