Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ester Amos Bulaya (41 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kuwashukuru baba zangu, mama zangu wa Jimbo la Bunda Mjini kwa unyenyekevu mkubwa, bila kujali umri wangu, bila kujali jinsia yangu, mkasema ng‟wana Bulaya ndiye chaguo sahihi la Jimbo la Bunda Mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushindi wangu umetoa fundisho kwa wale wote wenye kiburi cha kukaa madarakani muda mrefu. Pia ushindi wangu umetoa fundisho, wananchi wataangalia product bora inayopelekwa na chama husika na si ukubwa wa chama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nitoe pongezi kwa Msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni. Wale ma-senior kama mimi asilimia 30 tuliorudi, mnajua kwamba isssue si Mipango, issue ni utekelezaji wa Mipango. Issue si Serikali ya awamu hii, ni utekelezaji wa Serikali husika. Issue si Ilani ya 2015, ni utekelezaji wa Ilani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia tena mapinduzi ya viwanda. This time don’t talk too much, fanyeni kazi. Rais wa Awamu ya Nne alipokuwa akizindua Bunge, alisema mapinduzi ya viwanda, kwenye Ilani ya mwaka 2010 ukurasa 171, imezungumzia mapinduzi ya viwanda. Hatuhitaji tena mzungumzie, tunahitaji mtende. Tunataka mtende! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sio kwetu sisi tu, Taifa hili linatuangalia, tutembee kwenye maneno yetu. Wenzetu wanachukua Mipango yetu wanaenda ku-implement kwenye nchi zao. Please, wapeni Watanzania wanachokitarajia. Tuache kusema, tutende. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Wabunge wote waliozungumzia reli ya kati na naungana na hoja ya kuhakikisha tuna viwanda, tuvifufue vya zamani, tuwe navyo. Ni jambo la msingi sana, lakini leo hii tunazungumzia mapinduzi ya viwanda. Tumemaliza ujenzi wa VETA kila Wilaya? Mambo haya yanakwenda sambamba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ma-graduate wenye masters, wenye degree wale ni ma-superviser. Tunahitaji kuandaa product nyingine ya certificate, ya diploma tuipeleke kwenye viwanda. Tunatakiwa tuwe na VETA, VETA na mapinduzi ya viwanda yanaenda sambamba. China ilifanikiwa kwa mtindo huo. Please tuwe na VETA, tuwe na viwanda, tunatoa watu huku kwenye VETA tunaingiza viwandani tunatatua tatizo la ajira kwa vijana. Tupange kwa makini, tutekeleze kwa makini kwa maslahi ya vijana wa sasa na wajao, please mkaangalie tena. Tusiseme tu VETA kwenye kila Wilaya ziko wapi tumezungumza miaka mitano iliyopita, this time mara ya mwisho tuongelee mapinduzi ya viwanda Watanzania waone viwanda si maneno, do not talk too much, tendeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtakapoamua kwenda kuwekeza kwenye viwanda, kuna mmoja alisema angalieni na jiografia, sisi kwetu kule Kanda ya Ziwa hatuhitaji katani kule ni pamba, ng‟ombe na uvuvi. Hiyo niliyosema ya VETA mwenye degree ataenda kusimamia samaki wanasindikwa vizuri yeye hataenda kusindika. Mwenye degree, mwenye masters hataenda kutengeneza viatu atasimamia viatu vimetengenezwa vizuri, ni ushauri chukueni ufanyieni kazi. Hamtaimba tena 2020 hapa, fanyeni kazi siyo maneno, it is not about slogan ni utendaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mlikuja hapa na Maisha bora kwa Kila Mtanzania yako wapi? Leo hapa kazi iko wapi? Siyo maneno ni vitendo. Siyo tu wingi kwa kuandika kwenye Ilani mmeziandika sana tendeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tumezungumzia kuhusiana na Shirika letu la Ndege jamani kuwa na Shirika la Ndege ni ufahari tukiwa kwenye nchi za wenzetu. Tunapishana tu na ndege za Kenya, Rwanda, sisi tunasema tu tutafufua, tutafufua lini? Nchi ndogo kama Malawi wana ndege. Baba wa Taifa aliacha ndege tunahitaji ndege. Mnaenda Dubai mnapishana na ndege za Kenya, Rwanda na kadhalika tunahitaji ndege. Kuwa na ndege jamani unachangia pia kwenye sekta ya utalii, watu mnaosafiri mnajua. Ukishuka pale Kenya wazungu wote wanaishia Kenya halafu wanakuja Kilimanjaro, tungekuwa na ndege wangeshukia Dar es Salaam fedha zile wanazoziacha Kenya wangekuja kuacha kwenye nchi yetu lakini ndege moja, sijui mtumba kila siku tunazungumzia ndege, ndege ziko wapi? Kwa nia njema tutende ili tulitendee haki Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunapozungumzia sekta ya utalii watu wanajua utalii ni tembo tu, siyo tembo, wenzetu kule wametengeneza visiwa, sisi mashallah Mungu ametupa hatuhitaji kuvitengeneza, tunavitumia kwa aina gani vile visiwa? Tunaboresha maeneo yetu mengine ya utalii, tuna Mbuga pale ya Saa Nane, ukienda kule unaona Mwanza nzima jinsi ilivyo nzuri lakini cha kushangaa hata hoteli kule hatuna. Tungetengeneza huu Ukanda wa Kaskazini na Kanda ya Ziwa ungekuwa sekta ya utalii. Mtu anatoka Ngorongoro, anaenda Serengeti, anaenda Saa Nane anaenda kwenye visiwa vyetu ambavyo Mungu ametujalia. Wenzetu nchi nyingine wanatengeneza visiwa na maeneo ya utalii lakini sisi tunayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ashakum si matusi wengine wanasema visiwa vyetu wanaenda kujificha wake za watu na wanaume za watu. Visiwa vyetu tunatakiwa tuvitumie kwenye utalii ndugu zangu. Tunayaongea haya kwa uchungu mkubwa, Mungu ametupa mali hatuzitumii. Haya ni mambo ya msingi tumeyasema na Mwenyekiti wewe ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maliasili na Utalii. Watu wanakuja wanayalalamikia haya, mambo kama hayo lazima tuyaweke katika mipango yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie deni la Taifa, nakubaliana kabisa hakuna nchi isiyokopa. Kukopa ni jambo lingine, kwenda kuwekeza katika kile ambacho wamekikopea pia ni jambo lingine. Leo hii tunadaiwa US Dollar milioni 19. Nimesema kukopa siyo shida, je, tunazitumiaje hizo fedha tunazokopa? Tunakopa tunaenda kuwekeza kwenye eneo gani? Fedha zetu za ndani tunaweza kuwekeza katika maeneo ya huduma za kijamii hizi fedha tunazokopa twende ku-invest katika maeneo ambayo yatazalisha na tutaweza kulipa deni kwa mujibu wa mikataba tuliyoingia na kuondokana na mlundikano wa riba kama ambavyo upo humu kwenye ripoti. Hilo ni jambo la msingi sana. Tatizo hata katika hii Mifuko yetu ya Hifadhi ya humu ndani ambayo tunaikopa na hatuilipi, tunaenda kuwekeza sehemu ambazo hatuzalishi. Hilo ni jambo la msingi ukikopa nenda kawekeze eneo ambalo litakuwezesha kulipa deni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba mtende, msiendelee kuongea, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nianze kupongeza hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, wajibu wetu ni kuwashauri kama tunavyowashauri kwenye mambo mengine; mkitaka yachukueni, lakini mnapoyaacha na madhara yake yanatokea kama yaliyotokea kwenye kikokotoo na kwenye mambo mengine. Kwa hiyo, Waziri na Naibu Waziri Mheshimiwa Jesca Kishoa ambaye leo ni birthday yake wamefanya kazi yao, wamelitendea haki Taifa lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mbunge wa term ya pili, na tangu nimeingia kwenye Bunge hili Serikali ya Chama cha Mapinduzi haijawahi kutoa pesa za REA zote, mbali ya kwamba pesa zipo kwenye uzio na tunajua pesa zikiwekwa kwenye uzio zinatakiwa ziende zote kwa mujibu wa Katiba na kwa mujibu wa taratibu zetu tulizojiwekea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naanza na awamu ya nne; mwaka 2010/2011 tulitenga bilioni 56.883, zilizotolewa ni bilioni 114; mwaka 2013/2014 zilitengwa bilioni 53.158, zilizotolewa ni bilioni 6.757; 2015/2016 zilitengwa bilioni 420, zilizotolewa ni bilioni 141, sawa na asilimia 34; 2017/2018, awamu ya tano sasa ya majigambo mengi… (Makofi)

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: …zilitengwa bilioni 499, zimetolewa bilioni…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester, subiri. Taarifa Mheshimiwa Dkt. Mollel.

MHE. JOHN W. HECHE: Wanataka kuharibu Bunge hawa...

T A A R I F A

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kumpa dada yangu mpendwa taarifa kwamba ameanza…

(Hapa Mheshimiwa John W. Heche alizungumza bila kufuata utaratibu na bila kutumia kipaza sauti)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Heche, siyo vizuri unavyofanya.

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Charles Wegesa, tulia.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Heche, naomba utulie jamani na wenzio. Mheshimiwa Dkt. Mollel, naomba umalizie taarifa yako.

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kumpa taarifa dada yangu kwamba ameanza vizuri na ameonesha jinsi ambavyo kwa awamu ya nne kumekuwa na kwamba inatengwa hela lakini tunahitaji kufikia lengo hatufikii, ndiyo maana tunaweka miradi ya kimkakati, kama ya Stiegler’s na mingine ambayo itahakikisha tuna-boost viwanda na chanzo mapato ya ndani yaweze kuongezeka ili tuweze kubadilisha bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha kusikitisha wanaongea kizalendo wakidai kwamba ni makosa kufanyika hayo ambayo yangetusaidia tuweze kufikia lengo yeye analolitaka. Kwa hiyo, wakati tuna-address issues hizo anazolalamikia anapinga kwa hiyo tunafikiri dada yangu ungetusaidia sasa kuunga mkono Stiegler’s na nyingine ili mwisho wa siku tuweze kufikia lengo ambalo unataka tufikie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester, taarifa hiyo.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni uchanga wa kuingia Bungeni unamsumbua, ni njuka siyo size yangu, siwezi kumjibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndiyo trend ya Serikali…

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Nitaanza vibaya mama.

MHE. ESTER A. BULAYA …ya Chama cha Mapinduzi kushindwa…

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Halima Mdee yuko wapi kwanza nikushtaki kwake?

MWENYEKITI: Waheshimiwa naomba tutulizane, tusikilizane Waheshimiwa, Mheshimiwa Ester naomba uendelee tafadhali.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema, kwamba pesa zikiwekwa kwenye uzio ni tofauti na pesa zingine anazozisema yeye, hizi zinaenda kwenye matumizi maalum, lazima ziende zote, ndiyo hoja iliyopo hapa. Ziko kwenye ring-fenced, ndicho ninachokisema, na hiyo trend ilianza tangu Bunge lililopita mpaka hili la Serikali ya Awamu ya Tano bado hamjafanikiwa kutoa pesa zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu hii imejipambanua inashughulika na ufisadi, imeanza na mishahara hewa…

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MWENYEKITI: Kuhusu Utaratibu.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nasimama kwa mujibu wa Kanuni ya 64(f) na (g). Kuwa Mheshimiwa Mbunge ametumia lugha ya kuudhi na inayodhalilisha wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa anayechangia amemwambia Mheshimiwa Dkt. Mollel kuwa ni ushamba wa kuingia Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester, umezungumza maneno ya ushamba? Haya, endelea.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti…

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge mnaosema ushamba nitawatoa nje, Mheshimiwa Ester endelea.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee na mchango wangu.

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Amenivurugia ndoa yangu huyu unajua, Halima Mdee mke wangu halafu ukaolewa…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati pesa za REA…

MWENYEKITI: Waheshimiwa tuwe na nidhamu jamani, hebu Mheshimiwa Ester naomba umalizie.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati pesa za REA Serikali hii inachelewa kupeleka, lakini bado…

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti,…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Selasini.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Sasa Mheshimiwa Chief Whip amesimama bado mnapiga kelele ya nini?

Mheshimiwa Chief Whip endelea.

MWONGOZO WA SPIKA

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba mwongozo wako, kwanza kuhusu aina ya taarifa zinazotolewa hapa Bungeni, lakini pamoja na hayo, Mbunge anachangia lakini Mbunge mwenzake anawasha microphone na kutukana. Na bahati mbaya sana inawezekana Kiti chako hakisikii, lakini maneno ambayo yamesemwa ni maneno makubwa sana na yameingia kwenye microphone. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi naomba mwongozo wako; hivi hii miongozo inayotolewa kwa ajili ya dhihaka tu pamoja na matusi na nini, unairuhusu iendelee kwenye Kiti chako ili vilevile iamshe hasira za watu? (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Selasini, nimekuelewa. Waheshimiwa tutulizane. Waheshimiwa tulizaneni, wote Wabunge hapa mnaelewa vizuri Kanuni na mnajua nini mnafanya, kwa hiyo mnafanya makusudi, mnaposema wawili, watatu, wanne mimi huku sisikii kinachozungumzwa na mtu mmoja, siyo ninawaachia, ukiongea wewe na mwingine na mwingine hakuna kinachosikilizika, kwa hiyo, mimi nashindwa kutoa maamuzi. Ila ninyi Wabunge mnaelewa Kanuni na mnafanya makusudi, yeyote ambaye atakwenda sasa hivi kinyume atatoka nje hana ruhusa ya kuchangia, naomba umalizie muda wako.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mbali ya kwamba fedha za REA haziendi zote, lakini kumekuwa na ufisadi, kuna malipo hewa. REA imeipa Kampuni ya HIFAB fedha za ziada, zilizozidi, Dola za Kimarekani 81,000 na ushee wakati ilipaswa kulipa dola 9,000; na hili jambo halijafanyika mwaka 2010, 2011, limefanyika mwaka 2017 kipindi cha Serikali ya Awamu ya Tano kuingia madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni wizi kama wizi mwingine, wahusika wanatakiwa washughulikiwe na mpaka sasa hivi na kwenye hotuba yetu tumesema bado Dola za Kimarekani 44,000 hazijarudishwa ambapo huko Serikali hii inasema ya wanyonge ndiko pesa za wanyonge zinapigwa. Huko ndiko ambako tunahitaji umeme vijijini, huko ndiko ambako Serikali hii imewapa Wakuu wa Mikoa waanzishe viwanda; wakati kuna uchafu huu hivyo viwanda vitakamilikaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna ukaguzi ulifanywa kwa mikataba mitatu iliyogharimu shilingi bilioni 984 ambapo imegundulika vijiji 55 kwenye Mikoa ya Tanga, Mwanza, Arusha na Manyara tayari vina umeme lakini wakandarasi wamelipwa tena waende wakaweke umeme. Huu ni wizi, na tunaposema wizi hatuwezi kunyamaza eti tukachagua awamu, huu ni wizi kama wizi uliofanyika awamu zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji ukaguzi maalum ufanywe ili hiyo dhamira sasa ya kuzima vibatari mikoani huko na vijijini itekelezwe. Kwa hiyo tutahitaji majibu sahihi. Sasa kama vijiji 55 hivi, je, kwa nchi nzima tunaingizwa mkenge kiasi gani, huo wizi upo kiasi gani? Kwa hiyo haya lazima yafanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa pia na malalamiko kwenye suala zima la kuunganishiwa umeme vijijini. Wanasema wenye pesa ndio wamekuwa wakipewa kipaumbele katika kuunganishiwa umeme. Wananchi wa kawaida huko majimboni kwetu wanalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninapenda kulizungumzia ni kuhusiana na suala la TANESCO. Mpaka sasa hivi Shirikia TANESCO linajiendesha kwa hasara kwa bilioni mia tatu na. Kipindi cha awamu ya nne wakati inaondoka madarakani hasara ilikuwa bilioni 124, yaani kuna ongezeko la bilioni 122. Sasa tulitegemea Serikali hii inayokusanya kodi ingeenda kuondoa zile hasara na kuleta faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado madeni; madeni kutoka bilioni 700 mpaka bilioni 958 na TPDC peke yake inaidai TANESCO bilioni 340. Ndiyo maana Kambi Rasmi ya Upinzani tulisema shirika hili litakufa, sisi siyo wa kwanza, tumeshauri ligawanyeni, kuwe kuna mashirika mawili, limezidiwa uwezo na athari ya madeni, athari ya kujiendesha kwa hasara inakwenda kuathiri kwenye mtaji. Haya ndiyo ambayo tunayasema… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Taifa tunapoamua kupanga katika mipango mbalimbali ya kitaifa, dhamira ni kuhakikisha mipango inatekelezeka kwa lengo la kukuza uchumi wetu, kwa lengo la kuhakikisha tunaongeza pato la Mtanzania mmoja mmoja na kwa lengo la kuhakikisha tunaongeza ajira kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe unajua, katika mipango yote suala la Mpango wa Mradi wa Liganga na Mchuchuma ni takribani zaidi ya miaka 20 linaongelewa katika Bunge hili. Liganga na Mchuchuma ilikuwepo katika mipango yote. Lazima tujiulize Serikali ya Chama cha Mapinduzi mna dhamira, mikakati na malengo ya kuhakikisha mnamuondoa Mtanzania kwenye umasikini na mna lengo la kuinua pato la Mtanzania mmoja mmoja au tunafanya kazi kwa mazoea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imejaliwa kuwa na madini ya chuma takribani tani milioni 126. Tumejaliwa kuwa na madini ya makaa ya mawe takribani tani milioni 428. Leo tunajenga reli ili ule mradi ukamilike unatarajiwa kutumia shilingi trilioni 17 na katika hizo ziko pesa za mikopo lakini tunaagiza chuma kutoka nje wakati Mwenyezi Mungu ametupa chuma chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyozungumza kupitia Shirika letu la NDC ambalo lina hisa asilimia 20 na kampuni ya Kichina tumeingia mkataba zaidi ya miaka saba lakini hakuna kinachoendelea katika Mradi wa Liganga na Mchuchuma. Sheria ya Madini, kifungu cha 47(2) kimeweka wazi ukipewa mkataba na leseni unatakiwa utekeleze ndani ya miezi 18. Tuna hisa asilimia 20 kupitia NDC, kuna Mchina ana asilimia 80 amevunja sheria, anafichwa. Kuna interest gani, kuna nini kinajificha huku pesa tunakwenda kukopa nje, tunaagiza chuma kwa kukopa nje halafu kuna mtu tunambeba, tuna madini tumepewa na Mwenyezi Mungu, tuko serious? Halafu tukihoji mnatupa tu maneno, timizeni wajibu wenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi kule wa Njombe na Ludewa hawaendelezi maeneo yao. Wamesema wapishe eneo la mradi…

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester, upewe taarifa; Mheshimiwa Waziri nimekuona.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji anayeendelea kuwa Mradi wa Liganga na Mchuchuma una vipengele sita. Vipengele vitano vimeshafanyika, kimebaki kipengele kimoja ambacho kinahusu mkataba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii mikubwa ina maslahi makubwa kwa nchi. Unapoingia mikataba na mashirika ya kimataifa lazima uwe makini. Kwa hiyo, majadiliano yanaendelea na yapo katika hatua za mwisho kuhakikisha kwamba mkataba huu unakuwa na maslahi mapana. Kwa hiyo, anavyosema hakuna kinachoendelea siyo sahihi kwa sababu ina mambo sita, matano yameshafanyika, limebaki jambo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba apokee taarifa hiyo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya, pokea hiyo taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei taarifa, najua ni Waziri mgeni. Hili jambo tangu enzi za mama Mary Nagu, vipengele vitano miaka 20 brother? Hii ni taarifa ya sasa hivi ya Waziri na inasema hiyo kampuni haina uwezo wa kuwekeza dola za Kimarekani bilioni 2.9. Shame! Okoeni pesa za Watanzania, tunaagiza chuma kutoka nje, Mwenyezi Mungu ametupa chuma chetu; tunahitaji nini? Halafu unajibu majibu kama hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Ludewa, Njombe, maeneo haya takribani zaidi ya miaka saba wameshindwa kuyaendeleza. Mnasema Serikali ya wanyonge wakati kuna watu kule mnawasimamisha zaidi ya miaka saba hawaendelezi maeneo yao, hawajalipwa fidia, mnamlindwa mwekezaji mnasema maslahi ya nchi; yako wapi wakati huyu amevunja Sheria ya Madini, kifungu cha 47(2) miezi 18 imeisha, like seriously? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba mtimize wajibu wenu. Haya madeni wanakuja kuyalipa Watanzania. Kuna mtu alisema dunia ni chuma, chuma tunacho tunaagiza nje kwa hela za mikopo; kweli? Halafu tunakuja tunafanya mzaha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Najua Serikali imekwenda kuchukua pesa tena kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwenda kuwekeza kwenye viwanda. Hatukatai kuchukua fedha za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kuwekeza kwenye viwanda kama kuna dhamira njema na Serikali mnalipa hizo fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia Ripoti ya CAG, inaonesha hali ya Mifuko ni dhoofulihali, mifuko iko taabani. Ripoti ya mwanzo…

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya, upokee taafifa kutoka kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba mpaka leo napoongea hapa kama Waziri wa sekta, thamani ya Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii imeshapanda mpaka shilingi trilioni 11.510. Sasa kama thamani ya Mifuko hii imeshafika shilingi trilioni 11.510 mpaka sasa, hicho ni kiashiria kwamba sekta inakua na siyo inakufa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nani mwenye majukumu ya kusema kwamba sekta inakufa? Ukitaka kuwa na mamlaka ya kusema mifuko inakufa ni lazima ufanye actuarial. Sasa hivi ndiyo tupo kwenye huo utaratibu wa actuarial. Mtathmini ameshaanza kufanya utathmini wa Mfuko ya Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma, manunuzi ya Mtathmini kwa ajili ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa sekta binafsi yameshakamilika. Kwa hiyo, taarifa ya Mthamini ndiyo itakayokuja kutupa uelekeo mzima wa sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mamlaka haya Mheshimiwa Ester ya kusema kwamba mifuko imekufa kabla Mtathmini hajatoa ripoti anayatoa wapi? CAG anafanya ukaguzi wa mwenendo wa fedha, Mtathmini kwa vigezo vya Umoja wa Mataifa na Shirika la Kazi la ILO ndiye atakayetupa mwelekeo wa Mifuko na sekta. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ester asubiri, asianze kuwahisha shughuli mapema. (Makofi)

MWENYEKITI: Taarifa hiyo Mheshimiwa Ester Bulaya, unaipokea?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza amejichanganya mwenyewe, naye amejuaje hiyo thamani kama bado tathmini haijafanywa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tathmini ya kwanza kabla Mifuko haijaunganishwa Mkaguzi Mkuu wa Serikali wa kwenu amesema mifuko haina uwezo wa kulipa madeni yake pamoja na madeni ya wastaafu. Amefanya tena ukaguzi na wewe unajua tarehe moja hapa tulipitisha Sheria ya Kikokotoo ukaliahidi Bunge na wewe ukaponea chupuchupu akaondolewa yule Mkurugenzi mwingine, ukaahidi hapa Bungeni mnakwenda kufanya tathmini ya madeni, huu mwaka wa nne sister, hukufanya. (Makofi)

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri wa Nchi, taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua ni lazima tutoe taarifa kwa sababu watu wasipotoshe mambo humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tathmini ya Mtathmini wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii ilifanyika kwa mara ya mwisho mwaka 2016/2017. Tathmini ile tuliifanya baada ya kupata maoni kutoka kwa wadau mbalimbali na walitushauri namna ya kwenda kwenye merging. Tulipitisha sheria hapa ndani kwamba mwaka mmoja, miwili baada ya merging ndiyo sasa tutafanya tathmini yenye uhaliasia wa kujua baada ya merging mifuko yote na sekta inakwendaje. Sasa asichanganye tathmini ya merging na tathmini hii baada ya merging tunakwendaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo masuala mengine ya kupona au kutokupona siyo kazi yake, iko mamlaka ya kutathmini haya yote. Mimi nasimama kama Waziri wa sekta namwambia Mheshimiwa Ester, tathmini ni mbili; ya merging ilishakwisha, tunasubiri ya mwenendo tunaokwenda sasa hivi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya, taarifa hiyo, ipokee.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dada yangu atulie tu, hayo mambo mimi hayanihusu ila ninachomwambia, mlipe madeni. Mnakopa hamfanyi tathmini, wastaafu hawalipwi humu ndani kila Mbunge anapiga kelele. Haya, kwa tathmini tu aliyoifanya CAG Serikali mnadaiwa shilingi trilioni mbili na bilioni mia nne kumi na saba, fedha za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo sijazungumzia deni la PSPF, takribani shilingi trilioni 11, mliwaamrisha wawalipe watu ambao hawachangii. Leo kwenye viwanda 12 mmekwenda kuchota tena fedha shilingi bilioni 339 kuendelea kuwekeza huku mnadaiwa shilingi trilioni mbili.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MBUNGE FULANI: Eeeh.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri wa Nchi, tafadhali.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, utanisamehe sana. Unajua ni lazima Bunge hili lielewe mwelekeo wetu ni nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa sheria, kazi ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya kwanza ni kuandikisha wanachama, ya pili ni kukusanya michango. Huwezi ukakusanya michango ukaitunza benki eti isubiri tu watu watakapostaafu uwape. Kazi ya tatu ni kuwekeza na unapowekeza michango unaongeza thamani ya ile michango muda utakapofika uweze kuwalipa wastaafu kwa kuzingatia sheria na taratibu zinazowekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, siyo kweli kwamba Serikali inajichoteachotea tu, hapana. Serikali inawekeza kwenye uwekezaji wenye tija ili muda unapofika mafao yaweze kupatikana.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Sasa kama
anataka hiyo michango iwekwe tu benki bila kuongeza thamani utapata wapi fedha? Kwa hiyo, Mheshimiwa Ester aelewe hesabu hizi za hifadhi ya jamii, azielewe vizuri.

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Halima, haiwezekani taarifa juu ya taarifa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Ester Bulaya, unapokea taarifa?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei. Halafu anajua mimi nilikuwa Waziri Kivuli wa Sera na Uratibu wa Bunge, anajua nilivyomkimbiza humu ndani kupitia Sheria ya Kikokotoo na Mheshimiwa anazungumzia michango, anataka nije huko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta zenu za Kiserikali, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi mliacha kupeleka michango shilingi bilioni 85; Mfuko wa Hifadhi ya Jamii shilingi bilioni 61; Mfuko wa Bima ya Afya bilioni 24 michango mlichelewa ninyi ndani ya siku 30, unazungumzia michango? Nazungumzia mlipe madeni, muwekeze kwenye maeneo ya mikakati. Hizi pesa siyo zenu, ninyi ni wasimamizi, pesa hizi za wastaafu wa taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi hatuoni dhambi kila Mbunge akisimama humu kuna wastaafu wana miaka miwili, wengine miezi sita hawajalipwa halafu hela zao mlizokopa hamlipi, mnachukua zingine mnakwenda kuwekeza, kwanza mmefanya tathmini hivyo viwanda vinalipa; mmefanya? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipeni pesa za wastaafu wa nchi hii, wamelitumikia taifa hili kwa jasho la damu. Mnataka morali iongezeke kwa hawa waliopo kazini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya, muda hauko upande wako, muda umekwisha. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikikupendeza Bunge lako Tukufu liweze kuagiza Serikali ituletee taarifa sahihi ya miradi yote ya kimkakati inaendeleaje. Kwa sababu unakuta miradi mingi either tunajenga kwa pesa zetu mwenyewe au kwa mikopo ambayo mwisho wa siku Watanzania ndiyo wanakuja kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wewe unajua kwenye miradi mingi ya barabara Mkandarasi anapochelewa kukamilisha mradi, I mean Serikali inapochelewa kumlipa Mkandarasi na kusababisha mradi kuchelewa unakuta Serikali inalipa mabilioni ya shilingi kwa sababu mradi umechelewa kukamilika. Sasa nilikuwa nataka nijue status ya mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ikoje, tuliambiwa ngonjera ngonjera nyingi tu, lakini kwa habari nilizonazo sasa hivi mradi uko asilimia 45 na ulipaswa mpaka sasa hivi uwe asilimia 99 ambayo leo ni siku ya 834 mradi unapaswa kukamilika Juni 14, 2021. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukienda kwenye vipengele vingine unakuta kukamilika kwa ujenzi wa tuta kwenye bwawa ni asilimia 43 ambayo leo ilitakiwa iwe asilimia 88, kukamilika njia ya kupokelea maji kwenye mitambo sasa hivi ipo asilimia 57, wakati ilipaswa kuwa asilimia 94, kituo cha kupokea na kusafirisha umeme kazi mpaka sasa hivi ni asilimia 50 ilipaswa kuwa asilima 99, kuna mwingine kuna upande mwingine asilimia 29 ilitakiwa kuwa asilimia 98, hii ni kinyume na mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa lazima tuambiwe na kuna taarifa mradi huu ukaenda mbele zaidi kuliko mkataba, lazima tuambiwe kwa kuchelewa kukamilika kwa mradi huu kinyume na mkataba Serikali yetu itamtoza Mkandarasi kiasi gani kwa siku kwa sababu hizi pesa ni za Watanzania na mkopo...

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya ni taarifa unapewa.

T A A R I F A

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri wa msemaji anayeongea ningependa kumpa taarifa kwamba mradi huu ulichelewa kwa sababu nyingi mbalimbali, lakini moja ya sababu ilikuwa ni sababu za kimazingira ambazo zilipelekea kuwekana sawa na wadau wetu mbalimbali wa mazingira ili mradi ule uweze kutekelezwa katika eneo lile, lakini sababu ya pili ni uwepo wa COVID-19 ambayo ilichelewesha baadhi ya mitambo kuingizwa nchini kutokana na viwanda vingi duniani kufungwa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa yake.

MWENYEKITI: Sijakuruhusu Mheshimiwa Ester Bulaya. Sasa Mheshimiwa Ester Bulaya unapokea taarifa hiyo?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya kuchelewa yote yalikuwa ndani ya miezi sita ulitakiwa ukamilike kwa miezi 36, umeenda 44 na ndiyo mpaka hiyo Juni 14, 2022.

Kwa hiyo, walizingatia huku na deadline iko pale pale kwa hiyo tunachotaka tujue tutamtoza kiasi gani kwa kuchelewesha huu mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije kwenye kazi yenyewe, wewe unajua tangu niingie kwenye Bunge hili kila taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali imekuwa ikielezea hali mbaya ya mifuko yetu kujiendesha, kuweza kulipa mafao, lakini hii yote ni kutokana na Serikali kukopa bila kulipa madeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimesoma ukurasa wa 29 wa Mheshimiwa Waziri amesema atalipa Trilioni Mbili kwa non-cash bond, nikukumbushe Kamati yako ya PAC baada ya Serikali huwa inasema hatudaiwi kiasi hiki, hatudaiwi kiasi hiki, Kamati yako ya PAC Report ya 2014 iliunda kikosi kazi kuchunguza deni na ikaleta ripoti tarehe 10 mwezi wa Kwanza 2015 ikaonesha deni la 1999 ni Trilioni 7.1 mwaka 2014. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwa mbwembwe zote baada ya miaka 22 bila aibu fedha za watumishi tunaanza kupewa Trilioni 22. Sasa nikija kwenye deni kuu la mifuko mnalipa Trilioni Mbili, nikija kwenye deni kuu la mifuko ambayo ni Trilioni 19 mnahitaji miaka mingapi mkamilishe kulipa, deni la Mifuko Hifadhi ya Jamii ambayo huku ndiyo kuna hatma ya watumishi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya kwa sababu hivi kwanini tukikopa mikopo ya kibiashara nje mnakimbilia kulipa haraka kwa sababu mnawaogopa wale mabeberu, lakini pesa za wazawa wanazokatwa kwa ajili ya akiba baada ya maisha yao ya kulitumikia Taifa lao kwa muda mrefu kwenye 1999 tu baada ya miaka 22 mnatoa trilioni mbili mnadaiwa trilioni saba, bado huku kwenye Trilioni 19 kwa deni la ujumla sijui mtalipa kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikwambie, kwa taarifa nilizonazo, maana hapa tulikuwa tunaambiwa biashara ya actuarial, najua ya mwisho iliyofanyika 2016 ndiyo tumeambiwa Serikali inadaiwa shilingi trilioni 19. Inawezekana mambo hapa yameongezeka zaidi ndiyo maana mifuko inashindwa kujiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa taarifa nilizonazo, consultant amemaliza kazi tangu mwezi wa Tano, imebaki Serikali kutoa maoni, wanaficha nini? Wanaogopa kusema mifuko ina hali mbaya au deni limeongezeka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Juni, 2020 inaonesha Mfuko wa PSSSF ilikusanya ili michango shilingi trilioni 1.3. Ilikuwa inatakiwa kuwalipa wastaafu shilingi trilioni 1.5, yaani cash walikuwa nayo kidogo kwa mahitaji ya kuwalipa wastaafu kwenye Taifa letu. Walichofanya, walienda kwenye government Security wakachukua shilingi bilioni 300, wakaongezea shilingi bilioni 190 wakalipa wastaafu na nyingine ndiyo wakaenda kuwekeza. Aibu! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti,…

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Pokea taarifa Mheshimiwa Ester Bulaya.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tu nimwambie Mheshimiwa Ester Bulaya, kama Serikali iliweza kupata fedha na kuwalipa wastaafu, nadhani angepasa kupongeza kwamba kumbe Serikali ilipata fedha na ikawalipa wastaafu. Hilo ni suala la kupongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kumwambia Mheshimiwa Ester ni kwamba Serikali wala haina nia ya kuficha hiyo ripoti na siyo kweli kwamba Serikali inaficha hiyo ripoti ambayo Mtathmini Mkuu ameshamaliza kufanya utathmini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti inapokuwa tayari ina utaratibu wake katika kuiweka wazi. Naomba nilikumbushe Bunge lako Tukufu, ripoti hii ni mali ya wafanyakazi, mali ya waajiri, mali ya Serikali na Watanzania wote kwa ujumla, wala siyo ripoti ya Serikali. Sasa kwa taarifa yake, baada ya mtathmini kumaliza hiyo kazi, sasa hivi ndiyo tuko kwenye vikao vya utatu; wafanyakazi, waajiri na Serikali, ili kuitathmini hiyo ripoti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tu kumpa taarifa kwamba hayo maneno siyo kweli Mheshimiwa Ester Bulaya, kwamba Serikali inaficha hiyo ripoti. Nadhani ni lazima tuwe tunaweka mambo wazi na tuyazungumze kwa msingi wake. (Makofi)

MWENYEKITI: Unapokea taarifa Mheshimiwa Ester Bulaya?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei kwa sababu hili goma limeisha siku nyingi, huu ni mwezi wa sita wanakaa na taarifa yao, wanaficha nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumza hapa kwamba mfuko uko hohe hahe, lakini mbali na yote na kutokulipa madeni, wanaendelea kuwapa kuwapa mizigo ya kuendelea kuwekeza kwenye viwanda 35. Wakati hawalipi madeni, bado wanawatwika mzigo, wenyewe wanachokusanya wanakosa, leo mifuko imetoa shilingi bilioni 339 kwenda kuwekeza kwenye viwanda 12, wakati huku mifuko yenyewe inakosa fedha ya kwenda kuwalipa watumishi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi hapa uliongelea kitu kizuri tu, ukaelezea ni namna gani Sheria ya Kikokotoo kuwa mbovu mpaka ongezeko la watu wanaostaafu kwa hiari limeongezeka. Nikaenda kutafuta; sasa nikwambie, baada ya Hayati Rais Dkt. John Pombe Magufuli kutangaza kusitisha kile kikokotoo cha mwanzo na ile sheria kupita, ongezeko la watu wa fao la kujitoa limeongezeka na ongezeko la watumishi wanaostaafu kwa hiari imeongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kikokotoo kipya, watu waliokuwa wakistaafu kwa hiari ni 2,562; baada ya kikokotoo kipya watu 4,730 wa fao la kujitoa walikuwa wamelipwa shilingi bilioni 21. Baada ya sheria, wamelipwa shilingi bilioni 53. Wastaafu kwa hiari kabla ya kikokotoo walilipwa shilingi bilioni 158; baada ya kikokotoo, wamelipwa shilingi bilioni 352. Walikuwa wanawahi wachukue chao mapema kwa sababu wanajua Serikali hamtabiriki, hawajui mtakuja na hatima gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna haja kubwa sana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili hiyo Mheshimiwa Ester.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna haja kubwa sana ya kulinda maslahi ya watumishi wa Taifa hili. Tuacheni bla bla, tutimize wajibu wetu. Hakuna mgomo mbaya kama wa watumishi kwa sababu hawaoni wala hawezi kujisemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua ni lini Serikali kwanza, itamteua Kamishna wa Dawa za Kulevya ili kuleta ufanisi wa kazi katika Tume, maana ni muda mrefu tangu aliyekuwa Kamishna muda wake kwisha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwa nini Serikali mmeamua kupeleka fedha za methadon (MDH), badala ya kupitia kwenye Tume ya Dawa za Kulevya kama ilivyokuwa zamani? Serikali haioni kuwa fedha hizo zitakuwa hazifiki kwa wakati kwenye vituo husika vinavyotoa huduma hiyo ya methadon kwa vijana walioathirika na dawa za kulevya?
Tatu, kumekuwa na mkakati wa kuvuruga utaratibu mzima wa kuwarudisha vijana walioathirika na dawa za kulevya kurudi kwenye hali yao ya kawaida, ambapo wauzaji na wasambazaji wa dawa za kulevya huenda kwenye vituo vinavyotoa huduma ya methadon kwa kuwashawishi vijana kuanza kutumia tena dawa za kulevya. Kitendo hicho kinarudisha nyuma jitihada za kupambana na dawa za kulevya. Je, Serikali mna mkakati gani wa kuhakikisha mkakati huo unakwama?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii ya Ujenzi. Kwanza kabisa Waziri akija kutujibu hapa jioni, ningependa atufafanulie katika hizi fedha za maendeleo ni kiasi gani kinakwenda kulipia madeni ya Wakandarasi ambayo natambua yameanza kulipwa, ni kiasi gani kinakwenda kumalizia miradi tuliyopitisha bajeti ya mwaka jana na kiasi gani kinakwenda kwenye miradi mipya, isiwe kiujumla hivi. Tunaomba, mmesema hapo kazi na sisi tunataka tuwasimamie muifanye kazi kiufasaha, siyo jumla jumla hivi, aje atuambie, kwenye randama sijaona. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningetaka kulizungumzia na hili pia nitasema kama Waziri kivuli wa Sera, Uratibu, Bunge na mazagazaga mengine. Mwaka uliopita kwenye Mfuko Mkuu, Wizara hii ilipitishiwa bilioni 199, leo kwenye kitabu chake Mheshimiwa Waziri amekiri mpaka Aprili amepokea bilioni 600. Kwa utaratibu wa kuheshimu mihimili amepata zote na ziada, alimpitishia nani? Huku ni kuvunja Katiba na kudharau Bunge, alipata zote, kuna Wizara zingine hazijapata, kaka yangu Mheshimiwa Nape wamempa bilioni mbili, mwaka jana tulimpitishia bilioni tatu hizi bilioni 500 nani alimpitishia?
Mheshimiwa Naibu Spika, lazima Bunge liheshimiwe, lazima tufuate Kanuni, lazima tufuate Katiba, kuna Wizara nyingine hazipata hata asilimia 50, yeye amepata 200 tofauti na tuliyompitishia humu, hatusemi asipewe pesa, tunataka utaratibu ufuatwe ili kujenga nidhamu ya matumizi. Leo kuna akinamama kule wanaomba gloves tumepitisha bilioni mia na, amepata 600 nani kampitishia? Tunapoyasema haya tunataka tutengeneze nidhamu, hatuna hila, mimi mwenyewe nataka apate fedha, angekuja kuomba sasa hivi tupitishe leo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea, Mheshimiwa Rais wetu mtukufu, mpenzi sana amesema tunataka tujifunge mkanda tubane matumizi fedha nyingi ziende kwa wanyonge. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri naona kuna residential house, Ikulu, JK ametoka miezi sita iliyopita imeharibika lini? Kila mwaka hapa tunapitisha fedha za ukarabati, je, amemtuma?
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwambalaswa amesema ukimtazama moyoni dhamira yake ni kwa wanyonge, hizi fedha mngepelekea TEA aende akatengeneze miundombinu ya elimu. Sasa hivi Wahisani wamegoma kuleta pesa, kipaumbele siyo kujenga residential house Ikulu, tupeleke kwenye miradi ya maendeleo wangempa Mheshimiwa Nape, wangepeleka TBC, wangepeleka na maeneo mengine. Kipaumbele residential house Ikulu, Dar es Salaam? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, jambo lingine nimesoma ripoti ya CAG, kuna halmashauri tano zimetoa mikataba ya utengenezaji wa barabara zaidi ya bilioni moja na milioni mia saba bila kujua dhamana ya hawa Wakandarasi, kweli! Ndiyo maana kule kwenye Halmashauri zetu mtu anaomba tenda hana hata greda, kwa nini wasilime barabara kama mashamba? Huu ni wizi, lazima usimamiwe, tukisema wizi usimamiwe tunataka biashara hii ikome ili Jimboni kwangu kule wananchi wangu watengenezewe barabara, mambo yaende hatuwezi tukasema funika kombe mwanaharamu apite, halafu hapiti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nakuja Jimboni. Mwaka jana walitupa bilioni moja utengenezaji wa barabara ya kuanzia kwa kaka yangu kule Mheshimiwa Kangi, Kisolya – Bulamba – Bunda – Nyamswa, na hili nilimwambia Mheshimiwa Waziri, mwaka jana ilipitishwa kwa kiwango cha lami leo naona imewekwa kwenye changarawe, tuchukue lipi? Wananchi wa Bunda kuanzia Mwibara kwa kaka yangu kule Mheshimiwa Boniphace Mwita, tueleweje, ni kiwango cha lami au cha changarawe? Hata hivyo, Mkoa wa Mara umekuwa ukipewa fedha ndogo kila mwaka, Mheshimiwa Rais alivyoomba kura alisema hizi ni kiwango cha lami hapa mmetuwekea changarawe, lipi ni lipi? Maneno yanakwenda huku, vitendo kule, tuamini kipi hapa?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kulikuwa kuna ukarabati, upanuzi wa barabara kubwa ya kutoka Dar es Salaam kwenda Musoma, Mheshimiwa Waziri wananchi wangu waliridhia kupisha upanuzi wa barabara wameshafanyiwa tathmini huu mwaka wa nne pamoja na baba yangu Mzee Wassira nyumba yake iko Manyamanyama, mnawalipa lini? Sasa mtuambie hapa lini mnawalipa hawa? Yuko na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Gimano anadai humu, lini mnawalipa? Kuna wazee maskini mmoja babu yangu, mpaka amekufa jana hajalipwa, kwa nini mliwafanyia tathmini mpaka leo hamjawalipa, naomba majibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, Mheshimiwa Waziri Halmashauri yangu mimi ni mpya barabara nyingi haziko sawa, kupitia TANROADS Mkoa wa Mara mmejipanga vipi kuhakikisha hizi Halmashauri changa mnazisaidia. Kwanza kama mnavyojua Wilaya ya Bunda ni miongoni mwa Wilaya maskini, Wizara kupitia TANROADS Mkoa wa Mara mnajipanga vipi kuhakikisha hizi Halmashauri mnazipa support kuhakikisha barabara zinapitika.
Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kuna nyingine zimeshaanza kufanyiwa kazi kama Balili – Mgeta, namshukuru Mkurugenzi wa TANROADS Mkoa wa Mara na maeneo mengine ya Kangetutya, Manyamanyama, sasa hizi nyingine hizi mna mkakati gani wa kuhakikisha mnazisaidia ?Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Mchango wangu utaanzia pale kwenye taarifa aliyopewa mdogo wangu, Mbunge wa Igalula; kwamba tusizungumze mambo kiujumla jumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mosi, tutazungumza kiujumla jumla kwa sababu taasisi zimetajwa kiujumla jumla halafu sasa tutawasaidia kuwataja waliohusika. Naanza na ukaguzi maalum uliofanywa kwenye Mfuko wa Tuzo na Tozo na Kufa na Kuzikana katika Jeshi la Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kifungu cha 66(3) cha Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma Saidizi Sura Na. 333, kimeainisha kuwa Inspecta Jenerari wa Polisi ndiye mwenye mamlaka ya fedha kwenye mfuko huo. Mwaka 2018 mpaka 2020/2021 Inspecta Jenerari wa Polisi alikuwa Sirro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mfuko huu, umetajwa ufisadi wa shilingi bilioni moja. Anayeidhinisha fedha hizi, alikuwa Simon Sirro, mleteni kokote aliko aje apambane na hali yake. Hamuwezi mkafumbia macho hivi vitu. (Makofi/Vicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mfuko huu umeanzishwa kwa dhamira moja ya saidia Askari wadogo wa Jeshi la Polisi. Wakifiwa na wenza wao zisaidie zile familia. Wanaopambana na Jeshi, wanaopambana kwa damu na Jasho katika kulinda nchi hii kwa kupambana na majambazi, wakipata madhara hizi fedha ndizo ziwasaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfuko huu wanaochangia ni askari wenyewe kwa kufanya kazi ya ziada kulinda kwenye migodi, benki na taasisi mbalimbali; halafu wanatokea vingozi wao wana-take advantage kwa ile nidhamu ya kijeshi kwamba hawawezi kuhoji, wanawadhurumu askari wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuulize leo Sirro yuko wapi, si ni Balozi? Arudishwe aje abebe mzigo wake. Hakuna Bunge la kulinda watu wa namna hii. Kuna wengine wametajwa waziwazi, leo ni Naibu Katibu wa Maliasili na Utalii. Katajwa waziwazi, tena tu baada ya Ripoti ya CAG anapata promotion. Why? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo askari hawa mbali na fedha zao kutafunwa kwenye huu Mfuko wa Tozo wanaochangia kwa jasho lao kwenda kulinda kwenye migodi fedha zao hazijulikani zilipo. Halafu unaambiwa alikuwa tu anachukua anaidhinisha, anatoa BOT anapeleka huku, anatoa huku anapeleka huku. Kati ya Kombania 62 amapeleka kwenye Kombania tano tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za ulinzi wa nchi hii, askari wanatoa mikoa yote. Watu wanasema alipeleka kwa washikaji zake, mimi sijui. Askari wana uchungu, na ndiyo hawa hawa wakistaafu wanakuwa wanapata kikokotoo cha shilingi milioni 17. It is not fair, si sawa. Mimi ni Mbunge naenda kwa term ya tatu; tumekuwa tukijadili sana vitu hivi, vinakera. Haya, tuliwanong’onezaga nyie kuhusiana na ufisadi wa MSD hamkuchukua hatua mapema, CAG akasema. Wengine tuna uwezo wa kupata taarifa mapema. Haya mmempeleka wapi; nasikia amerudishwa Jeshini. Is it fair, mnataka tunyamaze? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukienda katika Mfuko wa Kufa na Kuzikana, mlezi ni IGP, na wa kipindi hicho alikuwa ni Simon Sirro. Ubadhirifu kwenye Mfuko wa Kufa na Kuzikana ni shilingi bilioni 4.6. Waheshimiwa Wabunge, fedha katika mfuko huu ni michango ya elfu tano ya kila mwezi ya watumishi wa Jeshi la Polisi. Walivyodai uitwe mkutano mkuu ili wahoji matumizi hakuna kilichofanyika. Miaka mitatu, mitano halafu leo nasikia wakati CAG anafanya uchunguzi walivyoenda kumhoji IGP msaafu anasema, huyo aliyehusika eti ametoweka; kweli, mtumishi wa Jeshi la Polisi katoweka na nyaraka? Mnataka tuyavumilie hayo? Aliyekuwa kiongozi wa ulinzi wa Jeshi anatoa amri; yeye anahusika na hivi vitu halafu mnampa Ubalozi. Arudishwe apambane na hali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi mwenye sifa tutampa; na ninachukua fursa hii, maana huu uchunguzi haukuanzishwa bure; aliye-engineer alikuwa Katibu Mkuu wa Wizara hii. Sijui leo yuko wapi, Mungu amsaidie. Labda alinusa harufu ya rushwa. Kwa unyenyekevu mkubwa na kuipenda nchi yake akaagiza haya yafanyike. Inawezekana akaondolewa lakini watu kama hawa ndio tunu ya kulinda, wanaonusa harufu za wezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, atakayefanya vizuri tutamsifia na atakayefanya vibaya, popote alipo aletwe apambane na hali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayasema haya kwa uchungu. Haya nije kwenye halmashauri. Ubadhirifu wa shilingi bilioni 11 ya makusanyo yaliyotakiwa kwenda benki kupitia POS, shilingi bilioni 11 watu wamekusanya wameweka mfukoni. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine baada ya kuona zimepelekwa hizi Mashine za POS kwa ajili ya kuzuia wizi; wengine walizima. Chamwino walizima mashine ya POS kwa siku 1,905, Uvinza walizima mashine ya POS kwa siku 1,133, Ushetu walizima mashine ya POS kwa siku 397, Sengerema walizima mashine ya POS kwa siku 185. Mnajua kwa nini wanafanya hivyo; ni kwa sababu tunawalea. Hawa wakurugenzi wapo. Halafu anakuja kwenye Kamati anakwambia, unajua tumewapeleka TAKUKURU. Tukawauliza muda gani wanadai miaka mitatu, kwa nini tusiseme kwamba TAKUKURU ni kichaka? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi bilioni 11 za makusanyo kwenye majimbo yenu watu wametafuana; halafu wanatuambia wanapelekwa TAKUKURU; wengine bado wapo kwenye vituo vya kazi. Halafu mnataka tuyanyamazie haya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka wakati Rais anapokea ripoti alivyozungumzia mikopo hii ya asilimia 10, fedha ambazo hazijakusanywa zimeongezeka kutoka bilioni 47 mpaka bilioni 88. Mchanganuo wake sasa, mchanganuo wake unaambiwa milioni 900 ni vikundi hewa. Milioni zaidi ya 700 eti vikundi watu wamechukua mkopo halafu wakagawana. Bilioni 2.5 eti vikundi sasa hivi havijishughulishi na kazi yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaambie, watoaji mikopo Mwenyekiti ni Mkurugenzi, yuko Afisa Maendeleo, yuko DT, yuko Afisa Mipango, inakuwaje kuna vikundi hewa vinapewa mikopo? Inakuwaje kuna vikundi vyenye thamani ya bilioni 2.5 eti havifanyi biashara? Inakuwaje eti kuna vikundi vya thamani ya milioni 700 eti watu wamepewa mikopo halafu wakagawana? Mnajua kwa kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kanuni ya mikopo imesema wazi kabla hujatoa mikopo, lazima ukatoe elimu, lazima utembelee vikundi, lazima ujiridhishe na biashara wanayofanya. Halafu wanakuja kuleta majibu mepesi kwenye pesa zaidi ya bilioni 88 ambazo zingejenga zahanati, ambazo zingejenga vituo vya afya, wako ofisini. Sasa namshauri Rais …

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Shaban Ng’enda.

TAARIFA

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa Taarifa dada yangu, Mheshimiwa Ester Bulaya, ambaye anazungumza kwa uchungu mkubwa sana tena kizalendo kwamba, mambo hayo ambayo yeye anayaona yana uchungu mkubwa katika ubadhirifu wa pesa za umma, ndio yanayowafanya Wabunge wa CCM waseme itungwe sheria ya kufanya watu wanaofanya hayo sasa wakatwe vichwa. Kwa hiyo, katika Bunge hili suala la ubadhirifu na wizi linawaudhi watu wote, Wabunge wote na wananchi wote wa Tanzania. Halina itikadi hili ndio maana Wabunge wa CCM wanasema tulete sheria ya kukata vichwa watu hawa. Dada yangu endelea. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester, Taarifa unaipokea?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa ikitoka kwa kaka, senior, lazima niipokee, najua uzalendo wake wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wakati muafaka tukamshauri Rais, tuanze kuangalia sifa za Wakurugenzi, uteuzi wake. Mkurugenzi ndio CEO wa Halmashauri, anatakiwa awe na weledi wa kutosha, isiwe tu tunateuana kwa ajili ya kutoa zawadi, matokeo yake ndio haya, watu wanashindwa kutimiza majukumu yao kulisaidia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Naunga mkono hoja taarifa zote tatu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia sekta hii muhimu sana. Kwanza kabisa kwa moyo wa dhati nichukue fursa hii kumpongeza Waziri, dada yangu Ummy Mwalimu kwa uteuzi wako. Tunaamini mwanamke akipewa nafasi hasa katika sekta ya afya ambayo ina changamoto kubwa sana zinazowagusa wanawake, sisi tunakuombea ili uingie katika historia ya kuondoa matatizo ya wanawake. Pia nichukue fursa hiyo kumpongeza kijana mwenzangu kwa uteuzi Dkt. Kigwangalla, naamini usipofuata siasa, ukifanya kazi kwa profession yako ya Udaktari utasaidia sana kuboresha sekta ya afya katika Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tatu, niwapongeze Chama cha Demokrasia na Maendeleo, Mkoa wa Dar es Salaam kwa kushiriki zoezi la kutoa damu kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili, kuwasaidia watoto waliokuwa wamekosa damu wakati wa kufanyiwa upasuaji wa moyo ili waweze kufanya hivyo. Tunaamini bila kujali itikadi zetu, tukifanya hivyo tutasaidia sana kuchangia kwenye benki ya damu.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ningependa unipe ufafanuzi kwa nini fedha za methadone zinapitia MDH (Management and Development for Health)? Nauliza hivyo kwa sababu mwanzo zilikuwa zikienda Tume na ilikuwa rahisi sana kufika katika hivi vitengo ambavyo wanatoa hizi dawa kwa ajili ya kuwasaidia wale walioathirika na dawa za kulevya. Sasa hivi imeenda MDH na nafikiri ni mlolongo mkubwa sana kuliko ilivyokuwa mwanzo.
Mheshimiwa Spika, pia hivi sasa hawa watu wa drugs wana mkakati maalum ambao nchini Italia watu wanaouza dawa za kulevya waliutumia. Baada ya kuona kwenye mianya mbalimbali wameanza kuziba na nichukue fursa hii kuwapongeza Kitengo cha Usalama wa Taifa wanaoshughulikia dawa za kulevya.
Mheshimiwa Spika, baada ya kuziba hiyo mianya, sasa hivi wana mkakati wa kwenda kuuza dawa za kulevya katika hivi vitengo vya kutoa dawa za kuwarudisha wale vijana. Sasa tunataka kujua kama mnajua mna mkakati gani wa kudhibiti ili hii methadone iwasaidie vijana siyo wanatoka kunywa dawa wanarudi katika chemba za kuwarudisha tena katika kutumia dawa za kulevya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pili, kitengo cha magonjwa ya watu wenye matatizo ya akili pale Muhimbili, hakuna wodi ya watoto wa matatizo ya akili, wanakwenda kuchanganywa kwa wagonjwa wengine, moja wanaweza wakaumiza wenzao au wao wakaumizwa, kwa hiyo, ni changamoto kubwa sana hakuna wodi ya watoto.
Mheshimiwa Spika, kingine hata katika hiyo wodi ya watu wazima tunajua watu wenye matatizo ya akili, ambao wanakwenda hawajawahi kutumia dawa, wako active zaidi kuliko wale ambao wameshaanza kutumia dawa.
Serikali ina mkakati gani wa kuongeza wodi na kuwagawa, wale walioanza kutumia dawa, wanaoanza kupona wanakuwa kwenye wodi zingine na hawa ambao bado hawajaanza kutumia dawa wawe kwenye wodi zao ili tuepushe madhara ya kuumizana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini ukipitia taarifa ya CAG, Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), mwaka jana kuna mzigo wa shilingi bilioni 4.6 umeingia bila kukaguliwa, hapo ndiyo zinaingia cerelac fake, zinaingia S26 fake, maziwa ya kopo, zinaingia sorry pads fake, zinaingia pampers fake, zinaingia juisi fake na kadhalika. Mwisho wa siku tunawaona kwenye TV wanakwenda kusema tumekagua vitu fake vilivyoingia, je, ni jitihada gani ambazo zimefanywa kudhibiti kwanza visiingie kabla ya kusubiri vinafika dukani na kuleta madhara kwa watoto na kuleta madhara kwa Watanzania wote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo lingine nililotaka kulizungumzia hapa kuhusiana na hospitali yetu ya Ocean Road, nakumbuka mwaka jana nilileta hoja binafsi na Mheshimiwa Waziri aliyekuwa Naibu Waziri Dkt. Kebwe alijibu yafuatayo; “tayari Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kununua mashine.”
Mheshimiwa Spika, leo napongeza taarifa ya Kamati imeeleza ni uzembe umefanywa na Serikali, ile mashine haijaja, mbali na kutambua jitihada ya kujenga maeneo ambayo zitakaa zile mashine. Mheshimiwa Waziri mashine zilizokuwepo, zile mbili ni mbovu, zinafanya kazi kupita uwezo wake. Kwa siku zinahudumia wagonjwa zaidi ya 300 na tunajua ugonjwa wa saratani ya shingo ya uzazi unavyomsumbua mwanamke na tunajua matibabu ya kansa yalivyo ya gharama. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini Ocean Road waliomba Bohari ya Dawa, dawa tofauti tofauti 53 wamepata 17 tu, sawa na asilimia 35. Tunaomba kuwe na mkakati maalum wa kuhakikisha fedha zinazokwenda Ocean Road ziwe ring fenced ziende zote, pamoja na dawa zinapotengewa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo lingine tuwe na mkakati sasa wa kutanua wigo wa matibabu katika kanda zetu ili ile Ocean Road isielemewe. Hata katika takwimu ukiangalia wengi wanaopata hayo magonjwa ni watu maskini wanaotoka kwetu kule Manyamanyama na maeneo mengine.
Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kuchangia, nimelizungumzia sana nikiwa Mbunge wa Viti Maalum kuhusiana na kupandishwa hadhi Kituo cha Afya cha Manyamanyama kuwa Hospitali ya Wilaya. Hili ni jambo la muda mrefu, tunajua kuna changamoto ya kukosa chumba cha kuhifadhi maiti, lakini kama unavyojua Halmashauri yetu bado changa, tunaomba Wizara mtusaidie na uingie katika kumbukumbu. Hili ombi tangu enzi za Mama Anna Abdallah na wengine, naamini kwako wewe ni jambo dogo halitakushinda. Tunaomba utusaidie wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini, akinamama wasihangaike sana iwe Hospitali ya Wilaya kwa sababu inahudumia hata Wilaya ya jirani pamoja na mikoa mingine.
Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine natambua umuhimu wa Mfuko wa Afya, ni kuboresha sekta ya afya na kuboresha vituo vya afya na natambua kuna ufadhili wa DANIDA pamoja na fedha za Serikali, kuna Halmashauri 23 hazifanyi vizuri, natambua zingine zilizokaguliwa kati ya 160, 138 zinafanya vizuri. Hizi 23 kutofanya vizuri na kufuata masharti zimesababisha hasara ya bilioni moja na milioni mia moja tisini na tisa.
Mheshimiwa Spika, hizi fedha zingeweza kujenga vituo vya afya vingine, hizi fedha zingeboresha katika sekta ya afya hasa kule vijijini ambako tunatoka sisi. Mfano Halmashauri moja tu, kwenye taarifa yake imesema imetumia milioni 55 kwenda kununua dawa na vifaa tiba, lakini katika ripoti ya CAG alivyofanya ukaguzi, wametumia milioni 31, milioni 20 ni wizi mtupu. Sasa tunaomba kuwe na ukaguzi wa mara kwa mara na uangalizi kuhakikisha hizi fedha zinatumika vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile tunajua kuna upungufu katika Mfuko wa Afya wa wafanyakazi 32,000 katika Halmashauri zetu na hawa wafanyakazi ni pamoja na wataalam, kule Mheshimiwa Kigwangalla ambako hakuna hata mlango wa kwenda kumfungia mfanyakazi wala mfanyakazi wa kumfungia, kule ndiko tunatakiwa tupeleke wataalam, tuepushe vifo vya akinamama wajawazito, tuepushe matatizo ambayo yanawakumba wananchi wetu wa vijijini. Huu Mfuko ni mzuri, nia njema lakini lazima tufuatilie mara kwa mara, fedha zinazotengwa zitumike kwa malengo husika, ili tuweze kutatua changamoto za afya katika Halmashauri zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na nipongeze hotuba ya Kambi ya Upinzani na pia nikupongeze kwa kusoma vizuri hotuba yako, lakini changamoto kubwa dada yangu uliyonayo, hicho ulichokisoma upate fedha na ziende katika utekelezaji. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi hii nami kwa dakika chache niweze kuchangia Wizara ya Nishati na Madini. Kwanza kabisa, ningependa Mheshimiwa Waziri atupe status ya umeme nchini ikoje? Kumekuwa na tatizo la umeme kukatika mara kwa mara. Tuliambiwa hakuna mgao, je, mgao umerudi kinyemela? Hapa Dodoma peke yake umeme ulikuwa unakatika kila Jumapili kuanzia asubuhi unarudi saa 12.00. Siku hizi unarudi saa 9.00 kwa sababu Wabunge tupo Dodoma. Tunaomba hilo utuambie. Pia atujibu, kwenye fedha hizi za umeme, kiasi gani kinaenda katika kumalizia viporo? Kiasi gani kinaenda kwenye miradi mipya? Hilo pia tunaomba atufafanulie, siyo hivi tu kama ilivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wale asilimia 30 tuliorudi humu ndani, mwaka 2015 nilipokuwa nikichangia Wizara ya Fedha, nilisema fedha zilizopaswa kwenda REA zimeenda kutumika kwenye matumizi mengine. Nilisema, Waziri kama huyo anaweza aka-survive kwenye nchi yetu. Kavunja Katiba, kavunja Sheria ya Bajeti, kavunja kanuni za nchi! Leo athari tunaiona hapa, miradi ya REA Awamu ya Pili haijatekelezeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti anasema, shilingi bilioni 70 ilikopwa, Serikali yetu sijui nini! Imevunja taratibu, hapa hakuna kutafuna maneno, wamekwenda kutumia fedha zilizokuwa kwenye ring fence. Maana ya kuwa kwenye ring fence, hazipaswi kutumika kwenye matumizi mengine. Leo tutamnyooshea kidole Mheshimiwa Muhongo wakati hatukumpa hela, watu wamekwenda kunywea chai na maandazi huko ofisini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niliyasema haya mwaka 2015 nikiwa Chama cha Mapinduzi. Leo Makamu Mwenyekiti wa Bajeti ameyasema. Tunapozungumzia haya jamani, kwenye mambo ya muhimu ya kuondoa Taifa letu kwenye giza, kweli tumeshindwa kuchukua maeneo mengine, tunaenda kuchukua fedha zilizowekewa uzio? Leo hapa kila mtu akisimama, vijiji vyangu vya Awamu ya Pili havijakamilika. Hakupewa hela. Pesa zimekwenda kutumika kwenye matumizi mengine. (Makofi)
Nawahakikishia Waheshimiwa Wabunge ambao mmeingia sasa hivi, kama tusipoibana Serikali, huu utaratibu ukiendelea, Bunge lako Tukufu linapitisha fedha, Serikali inaenda kutumia kwenye matumizi mengine, hatuwatendei haki wananchi. Tukatae Bunge hili kuwa rubber stamp, tuseme mwisho, tuazimie pesa za REA, ile trilioni moja tunayoipitisha hapa iende, mwakani tuzungumzie mambo mengine tena, siyo umeme vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, haya hayana Chama! Wabunge wengi nyie tunatoka vijijini huko, tunajua hali halisi ikoje. Mimi Jimbo langu la Bunda Mjini, baba yangu alikata Kata saba vijijini alijua zitamsaidia na ndiyo nimemchapa. Kata saba ziko vijijini kule, nataka umeme uwake. Kaleta Kata saba Jimbo la mjini, nimemkunguta huko ndiyo nimemshinda vibaya hajaambulia hata Kata moja! Ndiyo nasema hizo zote ziwake umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Babu yangu, hapa hakuna cha viwanda kama hakuna umeme. Halafu tunazungumza mambo kama haya, Waziri wa Fedha hayupo! Hayupo! Lazima awepo! Mambo ya msingi kama haya, mwenzake alikula, hakupeleka fedha. Tunahitaji fedha hizi tunazotenga kwa mambo yanayogusa maisha ya Watanzania. Leo Vijiji vyangu kule vya Kangetutya, Kamkenga, Guta, Nyamatoke, Miale kote huko kuwe na umeme. Sasa leo shilingi bilioni 70 zile hazikwenda, halafu tunaongea lugha nyepesi eti Serikali umekopa hela iliyokuwa kwenye ring fence! This is the shame. Mpeni pesa Mheshimiwa Muhongo tumalize biashara ya kusambaza umeme vijijini. Sasa tunakula bila kunawa halafu tunakuja kufanya kazi tena ya kupitisha kumalizia viporo hapa! Bunge letu lazima liwe kali kwa maslahi ya Taifa. Hii tabia iwe mwisho! (Makofi)
Mheshimiwa Waziri kingine, Jimboni kwangu Kata ya Kabasa Kung‟ombe kuna mgodi pale. Naomba tutembelee ule mgodi, wanafanya kazi katika mazingira hatarishi. Kwanza hauwanufaishi wananchi wa Kata ya Kung‟ombe lakini mazingira yale siyo mazuri, hawafuati taratibu, kemikali zinawaumiza wananchi wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kingine pale kwenye Kata ya Mjini, umeme kwa wananchi ni shida, gharama kubwa, wananchi wa Bunda masikini…
NAIBU SPIKA: Tunaendelea.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi nijikite katika masuala ya Jimboni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake najua wananisikiliza. Moja, kama ambavyo nilimsaidia Waziri wa Viwanda na Biashara babu yangu kwa wezi wale wa EPZ nawaambieni mkashughulike na wezi wa miradi ya maji, mmoja ni mtoto wa aliyekuwa kada wenu na Waziri mwenzenu wa zamani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siyo kama wale wanaotajataja wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa zaidi ya shilingi milioni 800 Kata ya Kabasa, shilingi milioni 800 pesa za walipakodi, huyu mtoto, maji hakuna, kashughulikieni hilo tatizo. Nyamswa kwa Boni niliwaambia, ameharibu Mtwara ameharibu na maeneo mengine, huu mradi mkubwa ndiyo usiseme kabisa ilikuwa kila Serikali ikiweka hela wanakata benki moja kwa moja kwa huu utapeli. Rorya kule walimfukuza, wananchi wangu wa Bunda wanataka maji, nimeshasafisha Baba yao nasafisha na uchafu wote, sitaki nataka wananchi wa Bunda wapate maendeleo, hilo limeshaisha, nadhani mmeshanielewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunda kuna njaa, Baba wa Taifa alisema anayeficha maradhi kilio humuumbua, tuna njaa. Narudia, Bunda tuna njaa au niseme tu lugha laini, tuna upungufu wa chakula kwa kata zaidi ya sita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, njaa hii siyo ya kujitakia, tatizo la tembo kuharibu mazao ya wananchi, dada yangu Mheshimiwa Jenista alishakuja kutembelea tukampeleka katika mashamba na moja ya shamba aliloenda kwenye Jimbo langu na akaahidi ataitisha kikao pamoja na Waziri wa Maliasili mpaka leo hicho kikao hatujafanya, dada yangu sijui kikao tutafanya lini, utanijibu uniambie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Bunda wamesema hawataki kuomba chakula, wana uwezo wa kulima msiwatengenezee njaa wasiyoihitaji. Tembo wenu wanatoka wanakula mazao kule sijui ndovu, sijui tembo, sijui mazagazaga gani mtajijua wenyewe, halafu tena tukiwaambia tuna njaa hamtaki tuseme tuna njaa. Naomba wananchi wangu biashara ya kuombaomba hawataki na ninyi mmesema Serikali yenu hamtaki kuombwa sisi hatutaki kuomba, mnatuchokoza wenyewe, tembo wenu wanakuja kula mazao yetu, marufuku. Nimeshasema hivyo na mtuelewe, tunaomba mlete chakula kwa sababu tembo wenu ndiyo wamesababisha matatizo yote haya. Hayo ndiyo yaliyonifanya nisimame nizungumze. Wananchi wangu wanataka chakula, kwa sababu kuna njaa iliyosababishwa na Serikali kwa tembo wao kuja kula katika mazao ya wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipompongeza dada yangu Mheshimiwa Esther Matiko kwa hotuba yake nzuri ambayo inaonesha wanawake tunaweza, hongera sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumwambia Mheshimiwa Maghembe kwamba tutakayoyachangia hapa ndiyo atatudhihirishia ule msemo wa Kinana kumwita ni mzigo au lumbesa ni kweli au atudhihirishie hapa yeye ni mwepesi kama tissue.
KUHUSU UTARATIBU....
MHE. ESTER A. BULAYA: Nasema hivi, kama „tissue’ linakwaza namaanisha „wepesi‟ basi „tissue’ litoke „wepesi‟ libaki pale pale. Atuambie kama yeye ni mzigo au mwepesi. (Makofi)
MWENYEKITI: Endelea.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka kujua, nilipomaliza uchaguzi nilienda Ngorongoro, sikwenda South Africa kama wanavyoenda wengine, kuna mbuyu pale una eneo kama sebule, majangili walitengeneza ndani ya hifadhi ya Tarangire. Nataka kujua, tangu Wizara yake imegundua nchi yetu imepoteza tembo wangapi? Yaani majangili wanaenda kwenye mbuga, wanatengeneza mbuyu unakuwa kama sebule na askari wapo halafu tunaambiwa baadaye ndiyo waligundua. Tunataka kujua waliohusika na eneo hilo walichukuliwa hatua gani? Hilo ni jambo la msingi. Akitujibu hayo, nitajua yeye mwepesi au mzigo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine limeongelewa kwenye Kambi ya Upinzani kuhusiana na kampuni iliyopewa kuwinda, Waziri ametoa barua tena wakati Waziri aliyehusika aliinyima. Miongoni mwa waliokuwa Wajumbe kwenye Tume ya Uwindaji jana alipokuwa akichangia Mheshimiwa Nsanzugwanko alisema watu wale walikuwa hawafuati taratibu na inasemekana walishaua mpaka na simba. Sasa ni sababu zipi ambazo Wizara hiyohiyo moja ina maamuzi mawili tofauti kwenye hiyo kampuni inayolalamikiwa haifuati taratibu, huyu ananyima kibali, huyu anakuja kurudisha, kuna kitu gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kimezunguka hapo? Yaani huyo mtu anachezea tu sharubu za Wizara anavyotaka. Tunaposema haya, tunayaongea kwa sababu hatuhitaji Serikali ichezewe na hao mapapa. Haiwezekani Wizara hiyohiyo moja mnakuwa na maamuzi mawili kwenye kampuni moja yaani mnapingana na Tume yenu ya Wanyamapori? Kweli, atujibu mzigo au mwepesi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, Waheshimiwa Wabunge tumekuwa tukichangia humu ndani kuhusiana na mambo ya wakulima na wafugaji. Jimboni kwangu nina hifadhi, wakulima na wafugaji, yote nayahitaji. Kama kiongozi, siwezi nikaja hapa nikasema nahitaji uhifadhi halafu eti najitoa wazimu nasema nawachukia wafugaji, sitakuwa natenda haki. Wala sisemi kwamba napenda wafugaji halafu niseme sihitaji uhifadhi, sitakuwa nalitendea haki Taifa langu. Mheshimiwa Waziri wa Maliasili hili hawezi akalimaliza kwa kauli, hawezi kulimaliza peke yako, lazima Wizara zote tatu zikae na tukubali kwamba tulikosea, hatukuwa na mpango bora wa matumizi ya ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Baba wa Taifa alisema kukiri kukosea siyo shida, ni mwanzo wa kujipanga upya. Taifa letu lilikuwa halijajipanga kwa future kwenye matumizi bora ya ardhi. Leo hii ukiwa unatoka Hong Kong ukapanda treni unaenda Guangzhou utaona upande huu ni mashamba ya kilimo na upande huu kuna mashamba ya mifugo, hakuna mwingiliano pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua hatujapanga matumizi bora ya ardhi na hawa wafugaji bado hatujawafatutia soko la kutosha. Tujiulize leo tuna viwanda vingapi? Tunalalamika wengi, tuna mkakati gani wa kuhakikisha wanafuga mifugo ya kisasa na wanapata soko ndani ya nchi yao kuliko kuja hapa kama viongozi tunapasuka humu ndani, hivi tukitoka nje tunaweza kulisaidia Taifa letu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ya msingi lazima Mheshimiwa Waziri wa Maliasili akae na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Waziri wa Ardhi ili kuona ni namna gani tunaweza tukalitatua tatizo hili lakini kwa Wabunge kutupiana mpira humu ndani hatuwezi kufika na tusicheze na vita ya ardhi, ni mbaya sana. Mheshimiwa Waziri, hili ni jambo nyeti, jambo linalohusu Taifa letu, kama tumeshindwa kugombana katika uchaguzi, hatuhitaji ardhi yetu ije itugombanishe. Lazima tutengeneze mazingira mazuri ya vizazi vyetu siyo kuja kugombana humu ndani ya Bunge. Sisi ni viongozi, lazima busara itutawale katika kutatua migogoro hii, siyo kwa kauli tu ondokeni, mnakowapeleka kuna malambo au mazingira yakoje? Hilo ni jambo la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala la tozo kwenye hoteli, nilikuwa Mjumbe wa Kamati, naomba jambo hili Mheshimiwa Waziri aliangalie kwa muktadha wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Esther amezungumzia hapa kwamba kuna shilingi bilioni tatu zinapotea lakini tangu kesi ilipokuwa mahakamani Serikali imepoteza zaidi ya shilingi bilioni nane. Leo Wizara hii inashindwa kukazia hukumu wakati Jaji amekuwa mzalendo kwa Taifa lake, kuna nini hapa au hawa watu wenye hoteli bado na wenyewe wanaichezea Serikali wanavyotaka? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la kusisitiza, duniani kote hakuna utaratibu wa double entry, utaratibu ni single entry. Mheshimiwa Waziri, mtalii anaingia akitoka lazima alipe tena, tunaona katika maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nije Jimboni. Nilizungumzia suala la wananchi wangu kuhusu tatizo la mamba, Naibu Waziri akajibu amekwenda kupeleka swali langu katika Halmashauri ya Wilaya, mimi niko ya Mji ndiyo maana alipewa yale majibu. Mimi mwenyewe ofisi yangu ya Mbunge nimehudumia zaidi ya wananchi wanne Mheshimiwa Maghembe, kuna tatizo hili na nashukuru Mheshimiwa Waziri alikiri kwamba ataenda kulifuatilia. Peleka tu watu wa kuvua hatujaomba pesa ili wananchi waondokane na tatizo hili la mamba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, wananchi wangu hawataki kuomba chakula. Wanalima lakini tembo wanakuja kuharibu mazao ya wananchi. Hawa nao wameingia kwenye hifadhi? Mheshimiwa Maghembe, please wananchi wa Mara wanaona haya kuomba, tunalima! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wangu wa Nyatwali, Tamahu, Serengeti, Kunzugu, Mihale, Bukole, Mihale nilienda na Mheshimiwa Jenista ameona mwenyewe shamba lilivyoharibiwa. Mkasema mtapeleka magari kule hawafanyi patrol, juzi tembo wamekula heka 20, please, tafuteni ufumbuzi wa kudumu. Watu hawafanyi patrol tuone ni namna gani hawa wananchi wataondokana na tatizo la kuliwa mazao yao. Namwomba sana Mheshimiwa Maghembe ashughulikie suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, wananchi wangu wa Kijiji cha Serengeti, Tamahu, Nyatwari wanataka kujua hatma yao maana wanatishiwatishiwa kuhama. Hawajapewa fidia, hawajashirikishwa na kuna maendeleo kule kuna shule, zahanati na kuna kila kitu. Haiwezekani mtu akaamka tu akawambia leo mnahama bila kuwashirikisha wananchi. Kuna wazee pale wa miaka mingi lazima haya mambo yawe wazi. Wanahama mnawapeleka wapi, kwa fidia ipi, mbona hamjawashirikisha? Hayo ni mambo ambayo nataka anipatie majibu ili nimpime yeye ni mzito au mwepesi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Mpango huu muhimu wa leo. Kwanza kabisa nichukue fursa hii kuwashukuru Wabunge wenzangu wa CHADEMA kwa kuniamini na kunichagua kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu na nawaahidi sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisaidiana hapa Bungeni na nimepata taarifa kuna karatasi zinatembea hapa upande mwingine wa kumchangia mpiga kura wangu Mzee Wassira na mimi Mbunge wake naombeni pia nishiriki kumchangia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa naomba niende kuzungumzia Mpango…
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Tunapopanga mipango kama Taifa lazima tupange maeneo yanayogusa watu wengi na katika Taifa letu maeneo yanayogusa watu wengi ni sekta ya kilimo, takribani asilimia 80 ya Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda wa miaka mitatu mfululizo tumekuwa tukipanga trilioni 2.7 kwenda katika sekta ya kilimo, lakini zikatengwa bilioni 371, zilizotoka milioni 250 sawa na asilimia tisa, sasa kama tunapanga kutoka trilioni 2.7 kwenye sekta inayoajiri watu wengi tunatoa asilimia tisa tuna dhamira ya dhati ya kumkomboa Mtanzania! Haya ndiyo mambo ya msingi Wabunge wenzangu tujiulize na hasa sisi tunaotoka Majimbo ya Vijijini ambayo yanaitwa Mjini leo hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipanga hapa huko kwenye sekta ya kilimo tufikie asilimia 10 hatukufika, tukapunguza asilimia sita hatukufika, ikawa asilimia 3.2, leo kwenye sekta ya kilimo iko asilimia 2.3, tunaenda mbele tunarudi nyuma. Tuna mpango kweli wa kuhakikisha hii sekta inaondoa umaskini katika Taifa letu! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka mitatu mfululizo asilimia tisa kwenye sekta inayowaajiri watu wengi, halafu tukija kuongea hapa watu tunapiga bla bla! Please Mheshimiwa Mpango naomba apange na atekeleze kama kazi yake ni kupanga ajifunze na kutekeleza ili haya mambo yaende katika hii sekta nyeti, Watanzania wanufaike nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimeangalia katika mipango mbalimbali, Serikali kupitia Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, hapa naongea kama Waziri Kivuli, inadaiwa trilioni saba, kwenye hii mipango sijaona mkilipa. Trilioni sita ziko PSPF, Mfuko ambao hali ni hohehahe, tukisema Serikali mtachangia kwenda kufilisi Mfuko huu, mtajibu nini? Miongoni mwa fedha hizo ni fedha za mikopo takribani miaka 10 hamjalipa, lakini hamna mpango wa kulipa. Serikali inadaiwa mbele, inadaiwa nyuma, inadaiwa kushoto, inadaiwa kulia, lini sasa haya mambo yatakwisha? Hakuna humu katika mpango, jamani hii Mifuko tunatambua kuna mambo ya msingi ambayo inachangia, lakini tunahitaji hii Mifuko isaidie wanachama wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inadaiwa trilioni sita katika Mfuko mmoja ambao tumeambiwa unakaribia kufilisika, huna mpango wa kuonesha unaanza kulipa lini na ni deni la muda mrefu, tunajua deni lingine mlilirithi kwa watu ambao walikuwa hawajaanza kuchangia. Sasa haya mambo lazima tuoneshe kuna mikakati dhahiri ya kulipa, ndiyo kwanza mnapanga kukopa tena, tena ndani trilioni 6.8 wakati tunajua mkiendelea kukopa ndani mzunguko wa fedha unakuwa finyu. Hali ya umaskini ni kubwa wananchi ni hohehahe, uchumi umeshuka, huko kitaa hali ngumu, Wabunge hali ngumu, kila mtu kapauka tu, pesa hakuna. Haya lazima tuyaseme. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha hili naomba nimwambie ukweli, duniani kote kama Waziri wa Fedha hakuwa stable nchi inayumba, hatuhitaji Taifa letu liyumbe. Tunaomba mipango inayopangwa itekelezwe kwa maslahi ya Taifa letu, ni jambo la msingi sana. Leo hii tunazungumzia masuala ya viwanda lakini ukiangalia huku hakuna connection yoyote kati ya sekta ya kilimo, sekta ya viwanda pamoja na Wizara ya Elimu na Wizara ya Mafunzo na Ufundi, hivi vitu vinakwenda sambamba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliwaambia kwenye bajeti tulijua basi leo mngeleta katika Mpango, hakuna. Tukitoka mnasema, tukibaki tukiwashauri mnasema, mnataka nini sasa? Chukueni basi hata haya mazuri maana unajiuliza haya hatukuwepo uchumi umekua! Mikutano ya hadhara mmezuia uchumi umekua! Mmetufukuza Bungeni uchumi umekua! Kwenye mipango mmeshindwa kupanga sawasawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Bunge, kama Taifa tunaomba tuweke maslahi ya Taifa mbele tusijiwekee sisi kulinda nafsi zetu wenyewe, tumshauri Mheshimiwa Rais vizuri. Hali ya uchumi haiko vizuri, bandarini kumekauka kila sehemu kumekauka. Tuliongea katika briefing hapa, leo hii Bunge ni aibu ukiangalia kule majani ile green yote imekauka sasa hivi shida kila kona, wananchi wana njaa, Wabunge wana njaa, kila sehemu kuna njaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwambia Mheshimiwa Mpango apange na kutekeleza, huko kwenye Halmashauri ndiyo kabisa, yeye asipopanga vizuri, asipotekeleza Wizara zingine na zenyewe hali yake ni ngumu. Kwenye Halmashauri zetu mpaka leo fedha hazijafika, kwangu pale Bunda Mjini kwa sababu nimeamua kuongoza…
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunda Mjini hata photocopy tu wanakuja kutoa kwenye ofisi ya Mbunge kwa sababu nimeamua kuongoza. Ahsante.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa nafasi; wanasema mnyonge mnyongeni haki yake mpeni. Kwa moyo wa dhati kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Jenista Mhagama, mimi mwenyewe, Dkt. Ndugulile ndio tulioanza kushughulikia dawa za kulevya humu ndani kwa kutunga sheria ya kupambana nao, sio kutafuta sifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba nizungumze yafuatayo, sipingani na watu wanaopingana na suala la kupambana na dawa za kulevya, wale wote wanaotaka kupambana na dawa za kulevya wasimuongopee Rais, tumshauri Rais amteue Kamishna wa chombo cha Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya ambacho tulipitisha sheria yake humu ndani na nilisema kabisa nimempongeza dada yangu Jenista Mhagama na Dkt. Ndugulile sisi ndio tulianza huu mchezo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tutakapohakikisha hiki chombo kinapata Kamishna kwa kumsaidia Mheshimiwa Rais tutakamata wale wanaoingiza dawa za kulevya, wale mapapa, hao wanaokamatwa sasa hivi waathirika wanatakiwa wapeleke Muhimbili na Mwananyamala wakapate tiba, wale ni waathirika sio kwenda sero. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo ndio nililotaka niliseme na mdogo wangu Makonda akitaka kupambana na dawa za kulevya aende magerezani akakutane na akinamama Leyla atamwambia mapapa ili tuungane wote kwa pamoja na tunamkaribisha katika hili lindi kuhakikisha nchi yetu inapambana vikali dhidi ya dawa za kulevya kwa sababu mimi mwenyewe mdogo wangu anayenifuata yupo Mwananyamala anakunywa dawa methadone. Kwa hiyo, ninachokisema nina uchungu nacho na nimekifanyia utafiti wa kina na nilileta maelezo binafsi katika Bunge hili Tukufu na ninashukuru Mheshimiwa Jenista akalisikiliza alipoingia tu katika hiyo wizara tukaleta muswada na tukatunga sheria nzuri sana ambayo leo hii katika watu watakaokutwa nyumbani kwao wanafunga zile dawa za kulevya kuna fine lakini wanaenda jela zaidi ya miaka 20. Kwa hiyo, tulianza hiyo vita kwa vitendo kwa kutunga sheria kali sio kwa kukamata waathirika ambao wanatakiwa waende wakanywe dawa kama ambavyo inafanyika hivi sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tangu mwaka jana mwezi wa kumi na moja hivi vituo vinavyorudisha watu katika hali yao ya kawaida, hawa waathirika ambao wapo sero sasa hivi, hivyo vituo tangu mwaka jana havijapokea watu wapya. Ningependa kujua kwa sababu gani hawajapokea watu wapya na inasemekana dawa ya methadone haiendi kwa wakati. Lakini pia mkifuata ile hoja yangu binafsi niliiambia Serikali ihakikishe hivi vituo viende nchi nzima, tusiishie Dar es Salaam peke yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunajua tatizo la dawa la kulevya yanachangia sana katika maambukizi mengine ya magonjwa ya HIV. Kwa mfano, watu tu wa kawaida maambukizi ya ugonjwa wa HIV ni asilimia 5.1; kwa watu ambao wanatumia dawa za kulevya ni asilimia 25 mpaka 50. Kwa hiyo, sio issue ya kuwapeleka waathirika sero, hili janga ni zito. Kwa hiyo, mtu anaetaka kupambana tupambane na mapapa na sio waathirika ambao wanawekwa sero badala ya kuwapeleka katika vituo vya kurudisha katika hali yao ya kawaida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na haya ni maazimio ya UN ya mwaka 2006 ukitaka kupambana na dawa za kulevya pambana na watu wale mapapa wanaoleta nchini, hilo ndio jambo la msingi. Kwa hiyo, nilitaka niliweke hili sawa; tusifanye siasa katika vita ya dawa za kulevya. Tusimwongopee Rais kwa kutaka kuhakikisha vyeo vyetu, tumwambie ukweli na ili tumsaidie Rais amteue Kamishana wa hii Tume maana tangu tulipoipitisha hii sheria hiki chombo hakina Kamishna. Hilo ndio jambo la msingi ili tuungane kwa pamoja tuhakikishe tunatokomeza vita ya dawa za kulevya hapa katika Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imesema Tume ya Kuratibu na Kudhibiti Dawa za Kulevya haina fedha, ni aibu kwa nini hawa watu wengine wasiojua haya mambo wasifanye vitu kienyeji kama hatuwapi pesa za kutosha, tuipe hii Tume pesa ipambane na huu muziki kweli kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna Mahakama ya Mafisadi, niliiomba Serikali hizi kesi zinachukua muda mrefu, kuwe na Mahakama Maalum ambayo itashughulika na hii mipapa ambayo wako ndani na haipelekwi mahakamani. Kuwe na Mahakama Maalum inayoshughulika na hizi kesi za dawa za kulevya, hilo ni jambo la msingi sana katika Taifa letu, lakini sio kutafuta sifa na sio kutaka kuhalalisha vyeo vyetu pasipo sababu katika janga ambalo linaharibu kizazi cha watu cha vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie kabisa Waziri anayehusika, hivi sasa hivi wale mapapa wanaoingiza wanataka kuanza kuangalia soko kwenye hizi centre zinazotoa huduma yaani dawa za methadone, wale ambao Serikali imeamua kuwarudisha katika hali ya kawaida wao sasa hivi wanataka kwenda kuwauzia dawa katika vile vituo. Serikali ina mkakati gani ya kuhakikisha hawa watu hawafanyi hivyo? Ni mbaya sana lakini sasa hivi baada ya kuona hii sheria kali na tumeweza kuhakikisha kwenye ile sheria zile kemikali na zenyewe tumeziingiza katika sheria kuwa ni moja ya makosa, sasa hivi zile kemikali hawa vijana wanatengeneza hapa hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mdogo wangu Makonda watafute wale vijana wanaotengeneza hizi kemikali tuanze ku-deal nao, wanatengeneza viwanda vidogo vidogo halafu wale waathirika sasa tuwapeleke kwenye vituo tusiwaweke sero. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami kwa moyo mkunjufu, napongeza kwanza hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwa yale mambo mazuri ambayo yameandikwa na tumeendelea kuyasisitiza, Serikali myachukue myafanyie kazi maana kazi yetu ni kuwashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napongeza Majiji yote na Halmashauri zote zinazoongozwa na Upinzani. Mbali ya ufinyu wa fedha lakini wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana na hiyo inaonesha ni namna gani Watanzania hawakukosea kutupa kura na tunawahakikishia wakiendelea kutupa kura, haya mambo ya kuwaza mawasiliano ya simu, hakuna. Sisi tutawaza flyovers zenye nafasi na underground. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, sasa naomba niende katika Jimbo langu la Bunda. Kwanza, natambua kazi nzuri ambayo inafanywa na TANROADs Mkoa wa Mara, lakini pia nashukuru kwa baadhi ya barabara kwenye Jimbo langu ambalo tayari zimeshapandishwa hadhi, ila tu Mheshimiwa Waziri najua yeye ni mchapakazi na alikuja Bunda. Kuna barabara ambazo hazijapandishwa hadhi katika mwaka huu wa fedha, please, naomba mwakani ziangaliwe ziweze kupandishwa hadhi. Naomba sana, kwa sababu bado Halmashauri yetu ni changa, inahitaji kulelewa na inahitaji support yenu.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hiyo ni Sazira – Misisi – Kitaramanka, barabara ya Bitaraguru – Kiwasi na barabara nyingine zote hizo tunahitaji zipandishwe hadhi ili ziweze kupitika ili akinamama wanapokwenda kujifungua waweze kupita katika miundombinu iliyo salama.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nizungumzie Mfuko wa Barabara. Katika Mamlaka ya Mji wa Bunda, mwaka 2016 tulitengewa shilingi milioni 710 mpaka sasa hivi zilizofika ni shilingi milioni 73 tu. Shilingi milioni 700 ndizo zilizokuwa zimetengwa, zilizofika ni shilingi milioni 73, tutazifanyia nini jamani?
Mheshimiwa Naibu Spika, ni asilimia ngapi hiyo? Kumi kati ya 100! Please! Halmashauri yetu ya Bunda ni changa; na ukizingatia kwenye hizi Halmashauri, vyanzo vya mapato Serikali Kuu mmevichukua ambavyo vingesaidia hizi Halmashauri changa kujitahidi angalau basi kukarabati hizi barabara. Hamkuleta pesa.
Mheshimiwa Naibu Spika, TANROADs Mkoa wa Mara na wenyewe ni kilio. Mkoa wa Mara barabara zinazokarabatiwa sasa hivi ni vyanzo vya ndani. Kwenye RCC iliyopita, mpaka tuliunda Kamati ndogo kuja Wizarani kudai pesa. Miaka mitatu mfululizo mnachelewa kutupa pesa, Mkoa wa Mara tumewakosea nini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nazungumzia Majimbo yote; na huu mkoa una historia katika kutafuta uhuru wa nchi yetu. Mara unazungumzia Baba wa Taifa, lakini leo hii Mkoa wa Mara, Makao Makuu ya Mkoa tukizungumza Uwanja wa Ndege, mara mnauweka katika ujenzi wa kiwango cha lami, mara mnautoa. Tatizo liko wapi? Please, tunaomba Uwanja wa Ndege wa Musoma ujengwe kwa kiwango cha lami, biashara ya kuuweka na kuutoa na kuanza kuukarabati kwa kiwango cha changarawe tumechoka. Mara ndege zinakuja, mara zinasimamishwa kwa sababu ya uwanja mbovu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa alianza kuusema Veda one, Veda two karudi. Sasa akaja tena Nyerere One; sasa sijui akirudi tena Nyerere two, ataendelea kuongelea huu uwanja!
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tunazungumzia barabara ya Kisolya – Bunda – Nyamswa; barabara ya Nata ambayo inatokea Musoma Vijijini kwenda Serengeti, barabara ya Tarime – Mtomara mpaka Ngorongoro; lakini pia tunataka hizi barabara ambazo zinaenda katika mbuga zetu, kama kweli utalii ndiyo unaongoza katika pato la Taifa, kwa nini sasa tusitengeneza barabara ambazo zinaenda katika hizi mbuga zetu ili watalii waongezeke, Serikali iendelee kupata mapato tuweze kufanya mambo mengine? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa pia nimeona kwenye kitabu chako, nakupa hongera, barabara ya Tanga – Saadani – Bagamoyo, isiishie kutengewa fedha, zijengwe kwa kiwango cha lami. Barabara ya kutoka Iringa kwenda Ruaha National Park, kutoka pale Tarangire, zote hizo ziwekwe lami ili utalii wetu ukue.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, nizungumzie tu barabara ya Iringa kwenda Ruaha, zaidi ya kilometa 120, leo hii watu wanashindwa kwenda kule. Mvua ikinyesha wanatumia zaidi ya saa manne na hii Mbuga ya Ruaha ndiyo mbuga ya kwanza Afrika Mashariki kwa ukubwa na ina wanyama wengi. Kwa Afrika ni mbuga ya pili kwa ukubwa, lakini ni miongoni mwa mbuga tano zinazochangia mapato ya Serikali. Sasa kwa nini tunashindwa kuweka lami kwenye hizi barabara ambazo zinaenda katika mbuga zetu ili kukuza utalii wetu? Hilo pia ni jambo la msingi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie fidia ya barabara ya kutoka Mwanza kwenda Musoma. Katika kipande cha Jimbo langu wananchi wamedai fidia kwa muda mrefu katika kupisha ule ujenzi na tena barabara ndiyo ilifuata nyumba za wananchi, siyo wananchi walifuata barabara, watalipwa lini? Hapa pia nimetumwa na mpiga kura senior, baba yangu Mzee Wasira, ana nyumba yake pale Manyamanyama, mlipeni. Lini sasa mtawalipa hawa watu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati ukarabati wa hii barabara unaendelea, imekwisha, haijakamilika, tayari barabara zimeanza kuharibika. Hivi hawa Wakandarasi mnaowapa tender mnatumia vigezo gani? Kabla tu barabara haijakabidhiwa, tayari kuna mashimo kama mahandaki. Juzi niliuliza swali, hii barabara ya Dodoma, hapa Dodoma Waheshimiwa Wabunge wenyewe mnajua katika maeneo yetu, kila siku zinakarabatiwa. Kule Ununio, barabara ile ya Mbagala kule Dar es Salaam na yenyewe hivyo hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hebu tuone ni namna gani hawa Wakandarasi wetu wanajenga barabara zenye viwango! Hilo ni jambo la msingi sana Mheshimiwa Waziri. Kama wanashindwa kazi, washughulikieni. Siyo kwamba Wakandarasi wanachezea tu Serikali; mmewapa tender, hawafanyi kazi kama vile ambavyo inatakiwa na fedha za Serikali zinaenda bure.
Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ni madeni ya Wakandarasi. Barabara nyingi zimesimama kwa sababu Serikali hamjalipa Wakandarasi fedha. Naomba sana… (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Mheshimiwa Waziri achukue, alikuja Bunda, tunahitaji Mkoa wa Mara tupate fedha za kutosha… barabara zetu. Ahsante sana.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza kabisa nishukuru katika Jimbo langu la Bunda kituo cha afya cha Manyamanyama tumepata gari la kubebea wagonjwa, ahsante sana; lakini katika yote usisahau kinahitaji kupandishwa hadhi. Imemshinda mama Anna Abdalah, Mwakyusa na ni sasa ndugu yangu Kigwangalla na Mheshimiwa Ummy dada angu mbali na kazi zote anazozifanya Manyamanyama tunahitaji iwe hospitali ya Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, tumekuwa tukizungumza humu ndani tutamsulubu Ummy, tutamsulubu Kigwangalla, lakini wote tunatakiwa tuibane Serikali itimize, Azimio la Abuja la kutenga asilimia 15 ya bajeti ya Serikali Kuu iende kwenye Sekta ya Afya. Hawa hata kama wawe na misuli ya kufanya kazi kiasi gani wasipopewa fedha, hawawezi kutimiza majukumu yao.

Mheshimiwa Menyekiti, hilo ndilo jambo la ukweli lazima tuseme, asilimia 15 na hapa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha upo na wewe na mama unalisikia hilo, lazima uhakikishe Azimio la Abuja na Tanzania tumesaini linatekelezwa, kwa sababu zikitengwa asilimia 15 angalau changamoto ya Sekta ya Afya nchini itapungua na imekuwa ni kubwa; kuna tatizo la madawa, kuna kansa ya uzazi, kuna matatizo ya ugonjwa wa akili ambayo yamesahaulika kabisa. Yote hayo hayawezi yakafanikiwa kama tusipotimiza lile Azimio la Abuja la kutenga asilimia 15 kwenye bajeti kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nchi za wenzetu South Africa, Zambia, kuna mambo ambayo wameyafanya, fedha za dawa na vifaa tiba zinatokana na matumizi ya kawaida, ambazo ni fedha ndani, ni Bunge hili sisi kuamua, taratibu siyo misaafu, tukihakikisha pesa za dawa tunaziweka katika fungu la matumizi ya kawaida, uhakika wa fedha zetu za ndani kwenda katika madawa na vifaa tiba utakuwa mkubwa. Hapa nimpongeze mdogo wangu Upendo Peneza, aliomba kuleta hoja binafsi katika Bunge hili Tukufu lakini hakupata nafasi. Kwa hiyo lazima tubadilishe utaratibu na sisi si wa kwanza, tukifanya hivyo, si tu tutakuwa tumetatua changamoto katika sekta ya afya, tutakuwa tumeokoa vifo vya akinamama na watoto na tutakuwa tumetatua matatizo mengi ambayo yapo katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine Mheshimiwa Waziri Vyuo vya Maendeleo ya Jamii. Kabla Wizara hii haijaunganishwa unakijua Chuo cha Kisangwa Bunda kina matatizo lukuki. Naomba chuo hicho mhakikishe kinapewa fedha za kutosha ili kutatua matatizo yaliyopo. Kingine gari ambalo limechukuliwa kinyume na taratibu, Wizara ilishaagiza gari lile lirudishwe, aliyekuwa Mkuu wa Chuo alijiuzia kinyume na utaratibu na barua ziko Wizarani, hakuna shangingi linalouzwa kwa shilingi laki tano, niliwaambia, naomba wizi huo mimi Jimboni marufuku sitaki nimeshaanza kusafisha. Kama ulikuwa kipindi hicho cha nyuma nimeshaingia mimi, sitaki biashara ya wizi Jimbo la Bunda, ni maendeleo tu. Naomba mambo hayo yote yazingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri na ndugu yangu Dkt. Kingwangalla, yeye ni Daktari na tulikuwa wote, back benchers huko. Suala la tatizo la afya ya akili pale Muhimbili, kila siku kati ya wagonjwa 150 mpaka 200 wanaenda pale, zile dawa ni ghali, sasa hivi wanachangia. Ukiangalia moja ya matatizo hayo yapo kwenye kurithi na yanachangia umaskini mkubwa, lakini kitengo hiki kimesahaulika kabisa. Mimi si daktari lakini wanasema matatizo yale kuna stage, lakini sometimes mgonjwa anaruhusiwa kwenda kwa sababu tu hakuna vitanda, hakuna maeneo ya kutosha ya kuwahifadhi wale. Kwa hiyo naomba mlifanyie kazi sana, tuwape…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mweyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina jambo dogo tu la kumkumbusha Mheshimiwa Maghembe, kwanza kabla ya yote najua moja ya mambo ambayo yanachangia kutoendelea kwenye sekta ya utalii ni pamoja na miundombinu. Mimi naomba nikuambie ni mtalii mzuri tu hata Easter yangu nilienda kula pale Ruaha National Park.

Mheshimiwa Waziri na Wizara ya Miundombinu hakikisheni hizi mbuga zetu zinapitika vizuri, barabara mpaka katika maeneo ya mbuga yapitike vizuri ili sasa tuweze kuvutia watalii wengi zaidi. Hilo ni jambo la msingi sana kama tunataka kupunguza kwanza gharama na kuhakikisha kunakuwa na watalii wa ndani zaidi; na wa nje kufika kirahisi katika mbuga zetu za wanyama, hilo ni jambo lingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niende jimboni; Mheshimiwa Waziri nilichangia mwaka jana na mwaka huu narudia, mimi napenda sana uhifadhi, lakini haya mambo yanategemeana na nilisema hatuwezi tukalinda mbuga zetu kwa mtutu. Watu ambao wanaweza wakawa walinzi wazuri ni wananchi wanaozunguka hizi hifadhi. Kule kwetu Mara, jimboni kwangu tuna Mbuga ya Serengeti lakini kila siku tembo wamekuwa wakitoka wakila mazao ya wananchi, wakiharibu nyumba za wananchi na kuua wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri hili nimekuwa nikilizungumzia sana. ukienda Kunzugu, Miale, Nyamatoke na maeneo mengine, ukija kule kwa kaka yangu Boni pia jimboni kwake na kwenyewe kuna matatizo hayo hayo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa niwapongeze Wabunge wa Afrika Mashariki wanawake waliochaguliwa jana, na bila kujali itikadi zetu tukiungana katika mambo ya msingi, tutakuwa tunaitendea haki nchi yetu. Pili, nipongeze kabisa jitihada zinazofanywa na Jiji la Dar es Salaam kwa kudhibiti huo wizi ambao umesemwa na aliyenitangulia chini ya UKAWA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa kama ambavyo tumeungana jana na kuweka historia ya kuwapeleka Wabunge wanawake wengi kwenye Bunge la Afrika Mashariki, ninaamini tutaungana tena kuibana Serikali kuhakikisha tunaitendea haki bajeti hii ya maji ambayo ukizungumzia watu ambao wanaumia katika suala zima la kutafuta maji ni mwanamke. Ninaamini tutaacha itikadi zetu pembeni ili tulitendee haki Taifa letu na tuwatendee haki wanawake wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina sababu kubwa za kusema hivi. Waheshimiwa Wabunge mwaka jana zilitengwa shilingi bilioni 937 fedha za maendeleo ni shilingi bilioni 915, zilizotoka ni asilimia 19 tu ya zaidi ya shilingi bilioni 900. Sasa tujiulize tupo kwenye kipindi hiki ambacho leo hii Waziri na Naibu wake shemeji yangu wanaomba tupitishie hapa bajeti. Hiyo asilimia 81 mtaileta lini kuwatendea haki watanzania na wanawake wa Taifa hili? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaposema tunaikataa bajeti naunga mkono hoja ya Kambi Rasmi ya Upinzani si kwamba tunawachukia, si kwamba hatutaki maji, no, tunaitaka Serikali na tunamtaka Waziri wa Fedha aende afanye anavyofanya mkae mjipange upya mjue sasa mtakapopata fedha mtuletee ili sasa sisi wanawake na wanaume wote na Waheshimiwa Wabunge wote ndio tuungane kuipitisha bajeti yenu. Haiwezekani tunasema tuna mkakati wa kuhakikisha tunamtua mwanamke ndoo ya maji kichwani mijini na vijijini, halafu mpaka leo zaidi ya asilimia 81 haijaenda kwenye Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilishasema nitasema ukweli, fitina kwangu mwiko. Nakupenda shemeji yangu na nakupenda mzee wa site, katika hili kwa sababu ninawapenda ninahitaji asilimia 81 mpate Serikali iende ikakae, ikatafute pesa iwape. Kuunga mkono hapa siwezi nikawapaka mafuta kwa mgongo wa chupa, hiyo si desturi yangu mimi. Si desturi yangu na kama mama, kama mwanamke na kama Mbunge wa Jimbo ambaye Jimboni kwangu..., nimesoma kitabu chako umeweka, umetenga hela. Mwaka jana ulitenga na miaka kumi iliyopita huo mradi ulikuwepo yaani leo wana Bunda kama ni birthday ni birthday ya kuanzishwa mradi wa maji kwa miaka kumi bila kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa biashara ya kutenga pesa ambazo hazifiki na kila siku nimekuwa nikisema mkandarasi huyo ni mwizi, amekataliwa Kigoma na Rorya. Mimi nilisema simtaki alienitangulia akawa ananibishia, wananchi wa Bunda wakasema mwana Bulaya jaga, nimekuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, wizi sitaki jimboni kwangu; wizi jimboni kwangu sitaki, silindi wezi, ninachotaka mimi ni maslahi ya wananchi wangu kwanza.

Mheshimiwa Waziri huyo mkandarasi ana madeni mengi, mkiweka hela kidogo badala ya kwenda kufanya shughuli za kukamilisha ule mradi wa maji ambao sasa hivi una miaka kumi haukamiliki, halafu mimi leo nije hapa hata kama nakupenda kiasi gani siwezi kukubali kuja kuunga
mkono wakati wananchi wangu wanaona tu mwaka wa kumi sasa hivi mradi wa maji haujakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri yetu ni changa lakini Mamlaka ya Maji Bunda ni class c, inapaswa kupata ruzuku Serikalini na ndiyo maana wanashindwa kulipa bili ya maji kwa sababu hampeleki fedha kwa mujibu wa taratibu anahitaji kupata ruzuku. Kwa sababu kuna neno kata, wanakata! Nilimuomba kaka yangu nashukuru umenisaidia na baba yangu Muhongo. Neno kata linatumiwa vibaya. Mnashindwa kupeleka fedha wakisikia kata wanakata bila kujua wanaathiri mamia ya wanawake na maelfu ya watanzania kwa kukosa huduma ya maji hicho kidogo ambacho kinapatikana, please! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine nadhani kwenye Hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani mmeambiwa kuna miradi hewa, nendeni mkaishughulikie kule, mkichelewa mimi nitawaumbua. Nilishasema kule kwa kaka yangu Mheshimiwa Bonny, mradi ule wa Mgeta – Nyangalanga amepewa mtoto wa mpigakura wangu senior, kala milioni 800 haujakamilika wakawa wanalazimisha apokelewe kinguvu, Makalla alikataa wakataka kumtumia DC nikamwambia wewe utaondoka wewe mradi hautapokelewa, haukupokelewa. Shughulikieni hawa wezi, msipowashughulikia nitawaumbua hapa, sicheki na mtu mimi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wizi Jimboni kwangu sitaki. Mradi wa Mgeta, shughulikieni. Wizi, conflict of interest, unatoa tender kwa mtoto wako, hana vigezo, kakataliwa maeneo kibao mpaka Mtwara kule, ondoeni wizi, nimesafisha mtu sitaki na mtoto wake, nataka mambo yangu yaende vizuri ili wananchi wangu wapate maendeleo kupitia binti yao, Ester ngw’ana Bulaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, naomba sana Mheshimiwa Waziri, mzee wa site na shemeji yangu wa Kantalamba, sana, mbali ya kwamba kuna hii miradi mingine imeanzishwa kama kule Rwabu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa Ester Bulaya.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kwa moyo wa dhati kabisa kutokana na changamoto za maji nchini, Taarifa ya Kamati imeelezea changamoto kwa kina na Waheshimiwa Wabunge humu ndani wote tunajua umuhimu wa maji kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea, nimesoma kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 174. Kwanza tu naomba nimwambie ukweli kwa sababu Mradi wa Bunda maji ni kama mtoto wangu niliyemlea tangu nikiwa Mbunge wa Viti Maalum, naujua vizuri sana na kwa sababu nataka kulisaidia Taifa hili, nitasema ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, hivyo vituo ambavyo vinasemwa hapa vilivyojengwa ni Nyasura, Balili Msikitini, Balili Stoo na Kunzugu. Makubaliano katika ujenzi wa mradi huu wa maji, vituo vilikuwa vianzie kwenye chanzo cha maji Nyabehu. Hilo halijafanyika na kilichotokea Mamlaka yetu ya Maji Bunda ikaamua kujenga kituo kimoja Nyabehu. Vituo vingine vilivyokuwepo kama Tairo ni kituo ambacho chanzo chake ni ile miundombinu ya zamani, siyo mradi huu mpya, hilo Mheshimiwa Waziri naomba ulizingatie kweli kweli. Mradi huu wa maji Bunda kilikuwa kichaka cha watu kula fedha za Serikali ambazo ni kodi za wananchi kushirikiana na watoto wa vigogo na wewe unajua. Lazima tuseme haya, tunahitaji hii miradi ya maji ikamilike mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, takribani miaka nane tunazungumzia chujio. Kuna habari nimezipata huko Wizarani kwako, aidha mmepigwa au mlikuwa mnataka kupigwa. Chujio la shilingi bilioni tatu mlikuwa mnaambiwa lijengwe kwa shilingi bilioni 12. Tunaipeleka wapi nchi hii? Kweli dhamira ya kumtua ndoo mwanamke kichwani itakamilika kwa ufisadi wa namna hii wakishirikiana na baadhi ya watendaji, ambao wengine mnawatoa Mtwara mnawaleta Bunda, mnawatoa Bunda mnawaleta Wizarani. Wizarani ambapo ndiyo kunasimamia miradi lukuki ya maji, hatuwezi kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mradi wa Maji tu Bunda unachukua miaka kumi na bado haujakamilika ina maana mnahitaji miaka 100 kwa ajili ya kukamilisha miradi ya maji katika majimbo kumi, hilo haliwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, huu mradi wa Bunda ni wa muda mrefu sana. Akisimama Mheshimiwa Boniphace atakwambia hivyo hivyo, akisimama Mheshimiwa Kangi atakwambia hivyo hivyo. Hatuhitaji Bunda Mkoa wa Mara kuwa kichaka cha wezi, tumechoka na hili tutaendelea kusema na tunaomba wachukuliwe hatua. Kwenye ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wananchi walisema na Ofisi yangu ilitoa ushirikiano na bado baadhi ya wakandarasi na watumishi wengine wanapeta. Wanakula na nani? Please, huu wizi sisi hatuhitaji, tunahitaji miradi ikamilike wananchi wapate huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwako kunahitaji maji, Waheshimiwa Wabunge wote wanahitaji maji katika maeneo yao na hili nasema kwa dhamira ya dhati. Itokee sisi Wabunge na Mawaziri tukatiwe maji miezi mitatu, tu-feel pinch ambayo wananchi wetu wanaipata ya kukosa maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazungumzia kumsaidia mwanamke kutua ndoo ya maji kichwani. Waheshimiwa Wabunge kwa miaka mitatu mfululizo mwaka 2015/2016 fedha zilizotengwa zikapitishwa na Bunge hili ni zaidi ya shilingi bilioni 485, zilizotoka ni shilingi bilioni 136 sawa na asilimia 28. Mwaka 2016/2017 fedha zilizotengwa shilingi bilioni 913, zilizotoka shilingi bilioni 250 sawa na asilimia 25. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka Aprili mwaka huu fedha zilizotengwa za maendeleo ni shilingi bilioni 673, zilizotolewa ni shilingi bilioni 135. Tunaenda mbele, tunarudi nyuma. Ile dhamira ya kuhakikisha mwanamke hatembei umbali mrefu kutafuta maji iko wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka mitatu mfululizo! Yaani badala ya kupanda, tunashuka. Asilimia 28, 25, 22, why? Halafu tunakuja hapa tunasema kweli tuna dhamira ya dhati ya kuhakikisha tunamaliza tatizo la maji katika Taifa hili. Kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko kwenye Majimbo ya Vijijini kwenye mahospitali yetu kuna operesheni hazifanyiki kwa sababu maji hakuna hospitali. Naomba hili jambo mliangalie kwa umuhimu wake. Wanawake wanateseka.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani sasa hivi bora umpelekee mgonjwa ndoo ya maji hospitalini kuliko chakula. Kama wawakilishi wa wananchi hali hii hatutaikubali. Hii figure nimetoa za miaka mitatu mfululizo, nikiwatajia hiyo ya miaka nane ni aibu tupu! Halafu bado tunakuja tunasema tuna dhamira ya dhati, kweli! Hata asilimia 40 tu tumeshindwa kufikisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikiliza sekta ya umwagiliaji; tunawahamasisha vijana graduate kwenda kulima kilimo cha umwagiliaji. Mwaka 2015/2016 mahitaji ni shilingi bilioni 400. Bunge hili tulipitisha shilingi bilioni 53 kwenda kwenye kilimo cha umwagiliaji. Fedha zilizotoka ni shilingi bilioni tano; asilimia 10, shame! Shilingi bilioni tano! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wangu wa Nyatwali wana project kubwa sana ya kilimo cha umwagiliaji; kwa pesa hii inawezekanaje? Wale wa kwa Karukekere kwa Mheshimiwa Kangi, Mgeta kwa Mheshimiwa Boniphace na maeneo mengine! Lazima tuseme haya mambo, hatuwezi kuyafumbia macho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira zimekosekana, vijana wamehamasika kwenda kuwekeza kwenye kilimo. Kwa pesa hizi! Haya mwaka huu Bunge tulipitisha shilingi bilioni 24, zimetoka shilingi bilioni nne tu kwenye kilimo cha umwagiliaji. Four billion, halafu tunakuja hapa kwa mbwembwe nyingi kwamba tunataka kuboresha kilimo cha umwagiliaji. Kweli tuko serious? Tunaguswa na maisha ya Watanzania? Tunaguswa na tatizo la ajira la vijana wa nchi hii ambao wameona Serikali haiwezi kuajiri, wameenda kujiajiri kwenye kilimo cha umwagiliaji, kwa pesa hizi tutazigawaje? Hata kama sungura mdogo kiasi hiki, hata mkia hauwezi ukatosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine miaka yangu yote nane ya Ubunge nimesikia upotevu wa maji DAWASCO ni ule ule asilimia 47. Ukienda kwenye ripoti ya CAG wamesema walishauriwa kununua chombo ambacho kitasaidia kudhibiti tatizo la upotevu wa maji. Mpaka leo kimya. Wizara yako inasemaje? Au kuna mradi wa watu hapa? Tunataka tujue.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Nishati
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Wizara hii nyeti. Naomba nianze na TANESCO na muda ukiniruhusu nitaenda maeneo mengine. Wabunge tuliokuwa katika Bunge hili kipindi kilichopita na ripoti mbalimbali za Kamati ikiwepo kamati ya Mashirika ya Umma ambayo mimi nilikuwa mjumbe, Mwenyekiti wangu alikuwa Mheshimiwa Zitto Kabwe, tulizungumzia namna gani TANESCO inajiendesha kwa hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya Serikali ya Awamu ya Tano haijaingia madarakani, TANESCO ilikuwa ikipata hasara shilingi bilioni124. Baada ya Serikali ya Awamu ya Tano kuingia madarakani, TANESCO inapata hasara shilingi bilioni 346. Hasara hizi zinatokana na upungufu wa maji ya uzalishaji umeme pamoja na gharama za uendeshaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hapo tu, Mwenyekiti wa Kamati ametoka kuelezea madeni ya TANESCO ambayo yamepanda kwa asilimia 23 kabla ya Serikali ya Awamu ya Tano haijaingia madarakani kutoka shilingi bilioni 738 mpaka shilingi bilioni 958. Haya si maneno ya Ester Bulaya, ukisoma ripoti ya CAG na imesema kabisa madeni haya hayana uwiano kati ya mali za Shirika la TANESCO pamoja na madeni. Kwa namna nyingine TANESCO imefilisika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati haya yanatokea kulikuwa na ushauri wa Kamati yetu chini ya Mheshimiwa Zitto Kabwe ya Mashirika ya Umma na taarifa mbalimbali ya Serikali kulikuwa na mikakati mbalimbali na ambapo nchi mbalimbali pia zinafanya, kwamba, hili Shirika ni wakati muafaka sasa likagawanywa yakawa mashirika mawili. Likawepo Shirika linalo-deal na masuala ya uendeshaji na lingine masuala ya uzalishaji, dunia nzima inafanya. Leo hii tusingekuwa tunaendelea kuzungumzia umeme wa kwenye vibaba wakati tuna-plan kuwa na nchi ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Hong Kong hawasheherekei miaka 50 ya Uhuru wanasheherekea miaka 50 umeme hata siku moja haujakatika kwenye nchi yao. Ni kwa sababu wana mipango mizuri katika uzalishaji na usambazaji. Sisi hatutakuwa wageni, South Africa wanafanya, jirani zetu Kenya wanafanya na hii mikakati ipo kwa nini, Serikali ya Awamu ya Tano hamtaki kufanya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mambo haya yanafanyika, hapo sijaenda deni la Standard chartered la Euro zaidi ya milioni 10 na gharama za kesi takribani bilioni 7.5, hilo naliacha wataongea wengine. Wakati haya yanafanyika na hali ya TANESCO ilivyo dhoofu, TANESCO pia inashindwa kukusanya madeni makubwa. TANESCO inaidai hospitali ya Tumaini dola za kimarekani milioni 9.4 sawa na bilioni 18 za Kitanzania na ni kodi ya pango. Tangu mwaka 1998 hawajawahi kulipa. Kulikuwa na kesi Mahakamani TANESCO imeshinda tangu mwaka 2016 na maamuzi ya Mahakama yanasema hivi, waondoke na kisha walipe TANESCO hizi Fedha. Mpaka hivi tunavyozungumza pamoja na maamuzi ya Mahakama TANESCO hawajachukua hatua yoyote pamoja na kuwa mfilisi wanahitaji fedha. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, lakini kingine TANESCO kwa masikitiko makubwa imetoa zabuni kwa mzabuni asiye na vigezo kinyume na mkataba. Masharti ya mkataba yanasema hivi, mzabuni awe na uzoefu wa miaka mitano, lakini sasa huyo mzabuni mwenyewe ana leseni ya kusambaza pembejeo yaani majembe, mbolea, kazi aliyopewa ni ya kusambaza nguzo ya umeme na keshakula dola milioni moja zaidi ya bilioni 2. Mkataba unasema awe na uzoefu wa miaka mitano na hii ni kinyume cha Sheria Na. 3 ya Mwaka 1972 ya Leseni na Biashara. Serikali ya Awamu ya Tano aibu, shame, shame, sasa haya tunayasema kwa sababu tunapenda nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati haya yanatokea mikakati ya kushindwa kugawanya TANESCO, mmeshindwa kulisimamia shirika vizuri, mmeshindwa kufuata ushauri uliotolewa na mikakati ya Serikali inashindwa kutekelezwa mnaenda kwenye mambo mengine ya Stiegler’s Gorge ambayo mmeitengea bilioni 700, hizo ni fedha zetu za ndani wakati hizo fedha mngepeleka kuboresha Shirika la TANESCO, mngeligawa mara mbili na pesa nyingine zingeenda kwenye REA. Hapa Mwenyekiti wa Kamati ameeleza wazi, mbali ya kwamba TANESCO inadaiwa, bilioni 700 zimetengwa kwenye Stiegler’s Gorge ambayo hatima yake hatuijui. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye REA kwa mwaka huu wa fedha, kwenye fedha zote za maendeleo hiyo Stiegler’s Gorge imetengewa karibia asilimia 40 ya fedha za maendeleo. REA ambayo at least mbali na changamoto zake imefanya vizuri asilimia 20 na bajeti iliyopita REA wamepata asilimia 49. Waheshimiwa Wabunge wote tunajua sheria, fedha zilizowekewa uzio hazipaswi kutumika kwa matumizi mengine. Fedha zinatakiwa zitolewe zote, kufanya hivyo ni kuvunja sheria na ni mfululizo wa Serikali ya Awamu ya Tano kutokutii sheria, amesema pale Mheshimiwa Nape, mnaendelea tena kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilitakiwa hizi pesa zitolewe zote, sisi Wabunge tunaotoka mikoani tunajua umuhimu wa umeme wa REA kukamilika. Timizeni wajibu wenu, tuache hizi mbwembwe ndogo ndogo halafu hapa mnasema mnataka kuwa na Serikali ya Viwanda, kwa mtindo huu, kweli? Haiwezekani! Mimi niwaambie baada ya kufikiria miradi mipya una uwezo wa kuacha legacy kwa kukamilisha miradi uliyoikuta ya umeme wa upepo, makaa ya mawe, tukamilishe haya kwanza halafu twende huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwepo wakati pori la Selou linatangazwa kuwa urithi wa Dunia nchini Qatar na dunia ikakubali kutusaidia kutupa fedha nyingi. Leo tunaenda kukata miti milioni mbili huko kwenye huo mradi halafu nasikia mkiulizwa mnasema ooh, tumechukua eneo dogo, jamani ni kama mwili moyo ni mdogo lakini mwili mkubwa, toa moyo kama binadamu utaishi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi yetu sisi Wabunge ni kushauri na kusimamia Serikali ifanye kazi yake ipasavyo kwa ajili ya vizazi vyetu vijavyo. Tunalipenda Taifa hili, hatuhitaji deni la Taifa liongezeke kwa sababu hakuna mipango thabiti ya kuivusha nchi yetu. Ukiona mpaka wengine tunasema hivi yametuchosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, timizeni wajibu wenu, acheni mbwembwe ndogo ndogo.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, kwanza kabla sijaanza kuchangia, lazima nisisitize mambo ya msingi na kama Bunge lazima tuvae viatu vyetu katika kuisimamia Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa na tabia ya kutofanyia kazi Maazimio ya Bunge na Kamati yetu tumesema, na changamoto inayotokana na kutofanyia kazi maazimio ya Bunge lako tukufu ni kusuasua kwa uwekezaji na utendaji wa mashirika yetu, hilo ni jambo baya sana na inaonesha Serikali hii inalidharau Bunge na tumesema kwenye Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Wabunge wenzangu, kuna suala la Kikanuni hapa kama ambavyo Kamati ya PAC na Kamati ya LAAC inavyofanyia kazi taarifa ya CAG sisi tunafanya kazi na Msajili wa Hazina. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyoongea hatujawahi kupewa ripoti na Msajili wa Hazina, hili ni jambo la kikanuni na tulipohoji tukaambiwa taarifa inakwama Wizara ya Fedha, aibu, mnatufanya sisi tushindwe kufanya kazi yetu vizuri kwa niaba ya Bunge kwa kusimamia mashirika na kuja kuishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na shirika letu pendwa la ndege, ni jambo jema kufufua Shirika la Ndege na hakuna mtu anayepinga. Lakini tujiulize tunafufua wakati gani, tuna mipango gani, kwa malengo gani ya ushindani wa kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika letu la Ndege kwa miaka mitatu mfufulizo wametengeneza hasara ya bilioni 316, mnajua ni kwa sababu gani! Shirika halina mpango wa kibiashara. Kwa nini tusibebe kitimoto, tusibebe mbuzi, tusibebe samaki kwenye ndege ya abiria? Haya mambo hayatutendei haki kama Taifa, kwa mfano, tumewekeza. Kwa mfano trilioni moja kununua ndege, lakini hivi karibuni tumeambiwa shirika letu limeingiza bilioni nne halafu limeenda kufanyia ukarabati ndege mbili kwa bilioni 13. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama haitoshi tuna upungufu wa marubani, Mwenyekiti wa Bodi alikuja kutuambia kwenye Kamati na ma-engineer yaani hivi ninavyowaambia marubani wa bombadier ndio wanaorusha dreamliner. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani ni kama dereva wa Noah mkabidhi basi la Shabiby abebe abiria, ndio mambo hayo! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka Shirika letu la Ndege lakini lazima mambo kama haya yafanyiwe kazi ili Shirika letu liwe na ufanisi, lijiendeshe kibiashara, lakini tuwe na usalama wa abiria wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu imewekeza takribani shilingi trilioni 54 kwenye Mashirika ambayo yana hisa kuanzia asilimia 50 mpaka 100, lakini imepata faida asilimia moja tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewekeza trilioni 54 faida kwa mwaka 2017 ilipata bilioni 800 sasa hivi, kwa hesabu za Juni, 2018 faida iliyopatikana bilioni 600 pungufu ya bilioni zaidi ya 200. Hizo bilioni 200 mngenipa bilioni tano ningemaliza mradi wangu wa maji Bunda. Hizo bilioni 200 hapa kila Mbunge ana matatizo lukuki au basi at least mngeenda kupunguza ahadi yenu ya shilingi milioni 50 kila kijiji ambayo hamjaitekeza, tangu muingie madarakani. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA): Mheshimiwa Mwenyekiti taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa.

T A A R I F A

MWENYEKITI: Ahsante sana, Mheshimiwa Bashungwa, Mheshimiwa Esther taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niu-junior unamsumbua sio type yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nililotaka kulisema hapa, tumesema Serikali haitoa mitaji kwenye mashirika mbalimbali. Nitoe mfano, tumeanzisha Benki ya Kilimo, Benki yetu ya Kilimo, lengo kubwa la kuanzisha ni kusaidia wakulima wetu, Benki yetu ili isimame ilikuwa inahitaji Mtaji wa bilioni 800, lakini sasa hivi ina bilioni 60 tu. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge mnakumbuka Kilimo ndio kinaajiri asilimia zaidi ya 70 ya Watanzania na kuna habari chini ya carpet kwamba benki hii, ambayo ina mtaji, wa bilioni 60 ndio alikuwa amepewa kazi ya kwenda kununua korosho za bilioni 900 wapi na wapi? Aibu haiwezekani na ni kwa sababu Serikali haifatilii mashirika yake haifuatilii vyombo vyake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na hili pia sijui mnabisha?

MHE. RICHARD P. MBOGO: Taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Mbogo.

T A A R I F A

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya taarifa hiyo.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei angesema hiyo pesa, hiyo pesa anayoisema ni mkopo kutoka TIB yaani Benki yenye mtaji wa bilioni 60 unaenda kukopa kuipa bilioni mia mbili naa; na hapa kwenye taarifa yetu tumesema kuna hatari ya benki kufilisika kwa sababu itashindwa kulipa deni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo nataka kusema hapa ni Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi kukopa bila kulipa madeni kwa taasisi zake na kusababisha utendaji mbovu wa mashirika TANESCO inadai zaidi ya bilioni mia mbili naa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye ripoti yetu utaona JWTZ inadaiwa Bilioni 8…

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa muda wako umemalizika Mheshimiwa Ester.

MHE. ESTER A. BULAYA: Ya kwanza eehe.

MWENYEKITI: Ya kwanza eeh, haya Taarifa Mheshimiwa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Na ulinde muda wangu.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa yake siipokei kwa sababu SUMA JKT, viongozi wa Chama cha Mapinduzi wamekopa matrekta na hamjalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, JWTZ inadaiwa bilioni nane, Wizara ya Maji - DAWASA inadaiwa bilioni sita, Wizara ya Afya
- Muhimbili inadaiwa bilioni 2 na maeneo mengine. Lakini tunajua mbali ya madeni, ambayo...

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA:…TANESCO inaidai Serikali, Shirika hili linashindwa kujiendesha, kwa sababu inashindwa kulipa madeni, na hela nyingi zipo kwa Serikali. Serikali inaua Mashirika yake…

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Ester taarifa tafadhali, Mheshimiwa Waziri.

T A A R I F A

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ndio nimesema moja ya maazimio ambayo hayajafanyiwa kazi kwenye taarifa yetu ya mwaka jana ni pamoja na Serikali kutolipa madeni, hapo sijazungumza madeni ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, takribani…

MBUNGE FULANI: Taarifa Mwenyekiti.

MHE. ESTER A. BULAYA: mmefilisi nyie.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya lazima tuyaseme kwa sababu wazalendo wanasema kwa lengo la kujenga, sisi wengine tusipokufa na ajali, tuna maisha marefu sana, tunahitaji Serikali itimize wajibu wake ili wananchi wapate huduma bora na mashirika yetu yafanye kazi, kwa ufanisi, lipeni madeni, acheni blah blah!

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa kama Bunge, nafikiri hatuwi wakali vya kutosha. Nadhani mnakumbuka miaka mitatu mfululizo Wizara hii imekuwa ikitengewa pesa kidogo sana, asilimia 18, 19. Bajeti iliyopita tumetenga shilingi bilioni 700 wamepata shilingi bilioni 300, hivi hizi zilizobaki zinafidiwa lini? Leo anakuja tena kuomba shilingi bilioni 600. Lazima Bunge tutimize wajibu wetu wa kuibana Serikali, unless otherwise tutakuwa tunamshambulia Mheshimiwa Prof. Mbarawa wakati Serikali haitimizi wajibu wake wa kupeleka pesa za kutosha katika Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maji hayana mbadala, umeme ukikatika leo, unaweza ukawasha kibatari, lakini ukikosa maji huwezi ukatumia maziwa kuoga, huo ndiyo ukweli. Huwezi ukatumia maziwa kunywa, kiu ya maji na kiu ya maziwa ni vitu viwili tofauti. Operesheni hospitalini zinakwama kwa sababu maji hakuna na ukiuliza sababu ni nini, Serikali haipeleki fedha za kutosha katika Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutakuja tutawasulubu hawa Mawaziri lakini pesa haziendi, Bunge sasa tutimize wajibu wetu, tuwe wakali, tuhakikishe pesa zinaenda na hiyo dhamira ya kumtua mama ndoo kichwani iwe kweli. Sisi tunaotoka majimbo ya mikoani, tunajua akina mama wana- suffer kiasi gani kwa kukosa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ninapozungumzia Jimbo la Bunda Mjini, shame. Kuna mradi wa maji pale una miaka kumi na moja haujakamilika yaani mradi wa maji na mwanangu Brighton wamepishana miaka mitatu. Mradi una miaka kumi na moja haujakamilika, Brighton yuko form one ana miaka kumi na nne, ni aibu. Kila siku unakuja kuzungumza kitu hicho hicho, ukiuliza tanki, chujio, chujio gani miaka kumi na moja inashindwa kukamilika watu wapate maji safi na salama? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni aibu, tunatesa wanawake, tunatesa akina mama vijijini huko. Wanatembea umbali mrefu wanakosa maji safi na salama. Mheshimiwa Waziri umeenda, naomba sasa usifike mwaka wa kumi na mbili, wananchi wa Bunda wamechoka kupata maji machafu. Hatuna mbadala, hatuwezi kunywa maziwa wakati tuna kiu ya maji, hatuwezi kuoga maziwa wakati tunataka kuoga maji, please. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mradi mwingine kwenye Kijiji cha Chakung’ombe, Mamlaka ya Mji wa Bunda ni Grade C haipati ruzuku Serikalini, kuna mradi wa shilingi milioni 800 umekamilika. Hata hivyo, kwa sababu Serikali haiwapi pesa mradi umeshindwa kujiendesha, umefungwa na gharama za maji zimepanda, kila siku wananchi wanalalamika. Haya mmeshindwa kukamilisha miradi iwezesheni basi Mamlaka hii iweze kutimiza majukumu yake. Gari haina, hamuipelekei ruzuku, mnategemea nini? Tunawapa stress tu watumishi, stress ya kuongezewa mishahara wanayo sasa wana-stress ya kupelekewa vitendea kazi ili watimize majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawaombeni sana Serikali hebu tutimize wajibu wetu na sisi Wabunge tutatimiza wajibu wetu kuisimamia hiyo miradi iwe na tija kwa sababu tunahitaji kumtua mwanamke ndoo kichwani. Tunamtuaje ndoo mwanamke kichwani kama hatupeleki pesa za kutosha? Nawaomba sana Halmashauri yangu ya Mji, Mamlaka ile ya Maji ipewe ruzuku iweze kutimiza majukumu yake, watu wana morali lakini Serikali haipeleki hela, please.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie. Mheshimiwa Waziri anajua kwamba Bunda tunalima pamba na kuna ginnery za pamba Bunda zimekufa. Wananchi wa Bunda wana stress kwenye mbegu, stress kwenye masoko, stress kwenye ginnery ambazo zilikuwa zinatengeneza ajira kwa vijana wengi wa Bunda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyozungumza Mheshimiwa Waziri maghala 24 ya kuuzia pamba na kuhifadhia yako kwenye hali mbaya. Mheshimiwa Waziri Misisi, Sazila, Mlimani Ligamba, Mheme, Taramanka, Balili, Kunzugu, Bukole, Mihale, Nyamatoke, Changuge, Jembemali, Mchalo, Jitume, Kisangwa, Tairo, Guta, Ibiti, Kunanga, Rwagu, Nyamilila, Kabasa, Kamkenga, Kalisumu, Bitaraguro, Kagetutya, Lindala, Kiwasi na Bunda Store; hizi zote zina hali mbaya. Pamba itaenda kuuziwa wapi? Itaenda kuhifadhiwa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kaka yangu Mheshimiwa Bashe najua ni mchapakazi, ametoka kwenye maeneo yanalima pamba. Wananchi wa Bunda baada ya kuona hivi, wanataka kujua Serikali mtakarabati lini haya maghala wanusuru kilimo hiki cha pamba ambacho ni kilimo ambacho kinachowasaidia wananchi wa Kanda ya Ziwa? Wananchi wa Mkoa wa Mara, wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Bunda.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuona kuna tatizo hili, wananchi wa Bunda wamejiongeza, wanaanza kulima alizeti. Hivi ninavyozungumza, Mheshimiwa Waziri wametenga hekta 10,000 kwa ajili ya kilimo cha alizeti, lakini hamjawapelekea mbegu. Sisi pale Bunda tunahitaji tani 30 tu za kuanzia na wamepanga kuvuna kilo 4,000,000 za alizeti ambazo watakuwa na uwezo wa kuzalisha mafuta lita 1,080,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa huku wameshindwa kujikamua, wamejiongeza kwenda kwenye alizeti, tena kwenye Kata ya Guta, Kabasa, Sazila, Waliku, Mcharo na Kunzugu. Naomba sana tupelekee mbegu. Kule Maafisa Ugani wako tayari, hata kama wengine wa pale Mji wa Bunda mnawachelewesha kuwapandisha madaraja. Sijui tumeelewana kaka yangu Mheshimiwa Bashe! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huku mtukarabatie maghala, lakini huku kwenye alizeti tunaomba mbegu. Tuna target ya kuvuna lita 1,080,000 za mafuta. Kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Bashe…. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika taarifa za kamati ambazo ziko mbele yetu. Kwanza kabisa nichukue fursa hii kumshukuru Kiongozi wa Kambi Rarmi ya Upinzani kwa kuniamini na kuniteua kuwa Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani. Hii inaonesha ni namna gani chama chetu kinavyotoa fursa kwa wanawake kushika nyazifa mbalimbali.v
Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwenye taarifa ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji. Mheshimiwa Spika, mosi, ningependa Mheshimiwa Waziri wa Maji akija kujibu anieleze. Mradi wa maji wa Bunda umechukuwa mda mrefu sana, na tatizo kubwa lilikuwa ni ufisadi wa
mkandarasi aliyekuwa anaendesha mradi ule ambao sasa hivi ni takribani miaka 12 na mradi bado haujakamilika.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara mkoa wa mara na akapata taarifa mbalimbali kuhusiana na mkandarasi huyu Nyakirang‟anyi aliyepewa kuhudumia mradi wa maji ambayo chanzo chake ni Jabeu.

Mheshimiwa Spika mkandarasi yule Waziri Mkuu aliamuru TAKUKURU imkamate kuhusiana na ufisadi unaofanyika kwenye mradi wa Bunda. Kama haitoshi Mheshimiwa Rais alifanya ziara Mkoa wa Mara na kwenye Jimbo la Bunda Mjini akaelekeza mkandarasi yule akamatwe na akafunguliwa kesi ya kuhujumu uchumi.

Cha ajabu, mkandarasi yule ameongezewa mkataba tena ili kumalizia mradi Bunda; kwa ajabu. Yaani mtu amefanya madudu yote, Waziri Mkuu amesema Rais ameenda amesema bado tu Wizara mnampa tenda mwizi ambaye tayari mlisha declare wenyewe kwamba huyu mtu ni mwizi na amechelewesha huu mradi. Ilifikia kipindi account zake zote zikafungwa, Wizara kipindi cha Maghembe kikamkopesha pesa mwizi; leo tena mnampa tenda? Kwenye moja ya mkataba wake ilikuwa pia aanze kujenga vituo, hajajenga mpaka sasa hivi; mnamuongezea tena mkataba kwa ajili ya kusambaza mtandao wa maji?

Mheshimiwa Spika, haya si maneno yangu nikiongea kitu nina uhakika nacho nakuona mdogo wangu unatikisa kichwa, nina uhakika nacho.

Mheshimiwa Spika, niliongea na kiongozi mmoja mkubwa Wizarani; akasema tumeona tumuongezee mkataba ili amalize; Mara mia kuvunja mkataba wa wizi mkampa mtu mwingine; alizoiba zinatosha ili wananchi wa Bunda wapate maji safi na salama huu mradi ni wa muda mrefu na kuchelewa kusuasua kwa mradi huu na nyie pia mnapata hasara. Ningependa nipate majibu sahihi kwanini mmerudia kumpa mkataba mwizi ambaye aliwekwa ndani na nyie mnasema ni Serikali safi mnashughulika na mafisadi, huyu fisadi mmemuongezea mkataba tena.

Mheshimiwa Spika, ningependa nizungumzie kidogo suala la pamba. Sisi wananchi wa Kanda ya Ziwa vitu tunavyovitegemea ni uvuvi ufugaji na kilimo cha pamba. Tangu nimeingia Bunge hili huu ni mwaka wa tisa kilio kikubwa cha wananchi wanaolima pamba ambacho Serikali ya Chama cha Mapinduzi kimeshindwa kutatua ni mbegu, bei, dawa ya kuulia wadudu na kulipa wakulima kwa muda mwafaka; imekuwa ni tatizo kubwa. Kama pamba ingewekewa utaratibu mzuri ingeleta fedha nyingi za kigeni, ingesaidia kumaliza matatizo mengine na kukuza uchumi wa taifa letu; lakini leo zao la pamba limeshuka. Sasa tunashindwa kuweka mikakati dhabiti ya kusaidia zao la pamba alafu tunakuja na maamuzi ya zima moto.

Mheshimiwa Spika, unakumbuka ilivyoletwa mbegu ambayo haina ubora hatima yake Serikali ilikimbizana kulipa fidia ya mabilioni ya shilingi. Kama tungefanya utafiti wa kutosha tukajua mbegu sahihi wakulima wangepatiwa leo tusingekuwa tunazungumza matatizo ya pamba.

Mheshimiwa Spika, kilimo cha pamba kinaanza mwezi wa kumi na moja lakini hivi tunavyozungumza mpaka leo wakulima hawajalipwa. Huyu mkulima anasomesha watoto, huyu mkulima ana mahitaji mengine. Tukileta takwimu hapa za wakulima wanaodai pamba si sawa, hawa nao ni binadamu. Si mnasema ni Serikali ya wanyonge? Wanyonge ni akina nani kama si hawa wakulima wanaotafuta wanaokopa kuhakikisha hawaombi wanatafuta pesa zao kwa jasho na damu? Hivi leo tukizungumzia mkoa wa Simiyu peke yake wanadai takribani billion nne; hapo bado hatujazungumzia Geita hatujazungumzia Mwanza, hatujaenda Shinyanga haujagusa Mara. Lipeni, na msimu unaanza mwezi wa tano. Jamani kama lilivyo zao la zabibu tegemeo kwa Mkoa wa Dodoma, kama ilivyo korosho tegemeo kwa Mkoa wa Mtwara na sisi wananchi wa kanda ya ziwa tegemeo letu ni pamba.

Mheshimiwa Spika, akisimama Mheshimiwa Raphael Chegeni atazungumzia pamba, akisimama Mheshimiwa Richard Ndassa atazungumzia pamba na nikisimama Ester Bulaya nitazungumzia pamba, akisimama Mheshimiwa Gimbi Masaba, akisimama Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki atazungumzia pamba na Mheshimiwa Ester Matiko atazungumzia pamba. Kilio cha pamba kimekuwa kikubwa; inawezekana ninyi Mawaziri hamjui hali halisi iliyoko kule chini.

Mheshimiwa Spika, please fanyeni utafiti wa kutosha msifanye utafiti wa kukurupuka. Fanyeni utafiti wa kutosha, lipeni wakulima kwa wakati ili tuhakikishe zao letu linakua. Kila siku kumekuwa na visingizie lukuki.

Mheshimiwa Spika, hivi vyama vya msingi ni tatizo, kuna rushwa huku. Sasa hivi kumekuwa na malalamiko, na mimi nimepata malalamiko kwenye Jimbo langu Kijiji cha Chagunge. Katibu wa cha msingi amekula pesa ya mkulima takribani milioni tatu.

Mheshimiwa Spika, vilevile havifanyi kazi kwa ufanisi, kuna mazingira ya rushwa. Mtu ili alipwe naye pia lazima atowe kitu kidogo. Tusipokuwa na mifumo mizuri huku juu inaenda kuambukiza uwozo mpaka huku chini, ndiyo maana leo vyama vya msingi navyo havitimizi wajibu wake na havifanyi kazi.

Mheshimiwa Spika, pia kuna tatizo kwenye suala la mizani kwenye vipimo. Tunajuwa inahakikiwa, tunajua; lakini leo hii mkulima anaenda kupima pamba yake, lets say ameweka kwenye shuka, kapeleka kg 15 anaambiwa hii shuka tu peke yake ina uzito wa kg. 3; ni wizi. Fuatilieni, pamoja na kwamba mmefanya uhakiki bado kuna rushwa ndogo ndogo zinamkandamiza mkulima wa pamba.

Mheshimiwa Spika, lakini kuna kitu kingine, nimepewa malalamiko kwa baadhi ya watu ambao wanalipwa. Anasema, anaambiwa ameingiziwa milioni 300…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ESTER A. BULAYA: …akienda kwenye akaunti anaziona akitoa anakuta milioni 20 wizi na utapeli ukemewe.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami niwatakie Waislamu wote mfungo mwema wa Ramadhani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa nikizungumzia sana suala la Serikali kuhakikisha inalipa madeni kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Leo nasisitiza Serikali mlipe madeni kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, hizi pesa siyo zenu nyinyi mnatunza tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jana nilikuwa najaribu kupitia ripoti mbalimbali, ripoti ya BoT imeonyesha 26% ya deni la ndani la Serikali wanakopa kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Ukienda kwenye ripoti ya CAG latest imeonyesha Serikali inadaiwa trilioni 2.7 bado haijalipa. Hapo sijazungumzia yale madeni ya kurithi ya kabla ya ile Sheria ya mwaka 1999 Serikali kuamuru madeni yalipwe wakati hakukuwa na michango. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hata mnapokopa kopeni kulingana na taratibu zilizowekwa na mifuko. Nitolee tu mfano Mfuko wa Bima ya Afya, Serikali ilikopa shilingi bilioni 220 kwenye sekta mbalimbali ikiwepo Wizara ya Mambo ya Ndani, 60% ya huo mkopo ambayo ni shilingi bilioni 132 walikopa hakuna makubaliano yoyote ya kimaandishi wala hakuna riba. Sheria Na. 5, kifungu kidogo cha (1)(f) cha Sera ya Uwekezaji wa Mifuko ya mwaka 2020 imeeleza bayana kwamba Serikali ikikopa ikope kibiashara na ilipe riba. Msipolipa riba mnachangia mifuko kukosa mapato, hilo hamfanyi. Hii ni kinyume kabisa na lengo kuu la mifuko kwa mujibu wa kifungu cha 33 cha Sheria ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya mwaka 2015. Kopeni, lipeni na fuateni taratibu. Hii ilishajitokeza hata kwenye mkopo wa UDOM kipindi hicho, mmechukua pesa kule hamkuingia mkataba, mkataba mkaingia baadaye, tuache! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala ambalo ni muhimu sana kwa wafanyakazi. Tumeliahirisha, liliwekwa kiporo baada ya sintofahamu iliyotokea mwaka 2018, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli akaingilia kati akasitisha kunyonya wafanyakazi kwa kikokotoo kibovu ambacho tulizungumza kwenye Bunge hili. Nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ukurasa wa 60 ameligusia kidogo lakini hawajasema bayana ni lini suala hili mtalitatua kisheria kwa kuleta mabadiliko Bungeni ili yale wanayoyataka wafanyakazi; kikokotoo chao kilichobeba hatma ya maisha yao baada ya kutumikia Taifa hili kwa jasho na damu kiwe cha neema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliwaambia mwanzo kikokotoo hiki mkiweke kwenye sheria kisiwe kwenye Kanuni ya Waziri hawakutusikia na hawakushirikisha wadau matokeo yake wakaleta kikokotoo kibovu cha 1/580 kuliko hata kile kilichokuwa mwanzo cha 1/540. Tulitegemea kingekuwa chini ya 1/540 basi hata ingekuwa ya 1/520 kama walivyokuwa wamependekeza awali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo mstaafu anastaafu unamwambia ile full pension unampa 25%, asilimia 75% utamlipa kidogo kidogo, haiwezekani kumpangia mtu pesa zake. Yeye mwalimu anayelipwa pension yake labda milioni 40 umlipe 25%, 25% ya milioni 40 akajenge, anasomesha huyo huyo mwalimu, bado hajaweka sawa mazingira mmeyaweka mabovu. Haiwezekani kwa nini tuwapangie mbona nchi za wenzetu wanachukua 50% wengine 75%, 25% siyo sawa kwa wafanyakazi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia michango haipelekwi, sasa hivi wastaafu wengi hawalipwi. Ukienda huko Mbeya utasikia kilio hicho hicho, Bunda na maeneo mengi hawa Wabunge wanajua wastaafu hawalipwi na hawalipwi kwa sababu michango maeneo mengi haipelekwi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano tu NSSF michango ya wanachama ya shilingi bilioni 284 mwaka mzima haijakusanywa. Ukienda pale Bima bilioni 24, ukienda Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi milioni 116 ziko nje wastaafu watalipwaje? Serikali hailipi madeni na michango haikusanywi, siyo sawa! Hizi pesa siyo zetu ni za watumishi wa nchi hii, tuwape morale, tuwarudishie kikokotoo chao, tukusanye michango yao ili wastaafu wetu wawe na uhakika wa kulipwa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia miaka mitano hawa watumishi sisi tunapanga mambo hapa wanaenda kuyatekeleza kwa kinyongo, five years hatujawapandishia mishahara. Wana stress ya kupandishiwa mishahara, wana stress ya kikokotoo kibovu, wana stress ya pesa Serikali wanachukua kwenye mifuko yao hawalipwi, wana stress wenzao wanaostaafu hawalipwi kwa wakati, wao waliokuwa kwenye utumishi hawajui hatma yao itakuwaje, siyo sawa! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala hili Mheshimiwa Hayati Rais JPM alisema, hivi sisi Wabunge tukimaliza tunapewa kitita chetu, hawa ambao tunatunga mambo yetu humu ndani wanaenda kuyatekeleza unawapangia 25%. Tutekeleze kazi hii kwa uadilifu, Mungu atulipe tuache legacy ya kuwatetea wafanyakazi wa Taifa hili ambao wanashinda usiku na mchana kutekeleza hiyo miradi mnayojivunia leo kwamba imetekelezwa, siyo ninyi ni hawa ambao mazingira yao ya kazi, hatma ya kiunua mgongo chao ni mabovu, tutimize wajibu wetu. Tulinde Taifa letu kwa kuhakikisha haki za wafanyakazi zinakuwa nzuri. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Wewe utakuwa shahidi, duniani watumishi ambao wanatoa huduma kwa wananchi na hasa kazi zao ngumu wamekuwa wakilipwa vizuri sana. Ukienda Marekani, Uingereza, Afrika Kusini na maeneo mengine, Walimu, Madaktari, Manesi na Polisi na vyombo vingine vya usalama wamekuwa wakilipwa vizuri, mazingira yao ya kazi yakiwa mazuri, pamoja na makazi yao kutokana na kazi ngumu wanazozifanya lakini na risk wanazoweza kukutana nazo kwenye kazi wanazozifanya.

Mheshimiwa Spika, mbali na changamoto za kiutendaji, lakini Polisi wetu wamekuwa wakilipwa mishahara midogo, hasa Polisi wa chini. Lakini sio tu, nyumba zao, ofisi zao ni aibu kulingana na mzigo waliopewa wa ufanyaji kazi katika Taifa letu. Nikitolea mfano pale Buhigwe, najua sasa hivi watakwenda kufanya kwa sababu ndio anakotoka Makamu wa Rais. Kuna muda Polisi walikuwa anafanyakazi kwenye matenti, kuna muda walikuwa wanatumia Ofisi ya Mtendaji wa Kata, lakini kuna wakati mwingine walikuwa wanakwenda kuchapisha documents mtaani. Hivi kuna siri za nchi au za kiupelelezi zinazoweza kuwa salama! Lazima tuboresha mazingira ya Jeshi la Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tumesema tunataka jeshi letu liwe la kidijitali lakini leo computer imekuwa anasa, sio hitaji la msingi. Unaweza ukakuta Makao Makuu ya Polisi, nenda Wilayani, nenda mkoani kwa Bunda pale jimboni kwetu, maana nikisema langu italeta mgogoro, Jimboni kwetu pale Bunda, utakuta ofisi ya OCD ndio kuna computer, kwa OC-CID na traffic ziko computer tatu. Leo sisi hapa tuna Ipad kwa sababu tunataka twende na teknolojia na wenzetu duniani wanavyokwenda. Tubadilike tufanye jeshi letu liwe la kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija kwenye Jimbo la Bunda Mjini. Pale Jimbo la Bunda Mjini ndio Makao Makuu ya Wilaya ya Bunda ambayo ina majimbo matatu, Bunda Mjini, Bunda Vijijini na Mwibara. Kituo cha Polisi cha Jimbo la Bunda Mjini ni aibu, hakuna nyumba, wanakaa mtaani, hata hizo nyumba chache tu zilizokuwepo ni aibu. Hivi leo Sajenti anapewa labda chumba kimoja kwa sababu cheo chake kidogo hatakiwi kuwa na familia! Akiwa na watoto walale wapi, sebuleni? Wanandugu wakija. Please, tuwatendee haki hawa askari wetu ambao wanalinda Taifa hili kwa jasho na damu.

Mheshimiwa Spika, nilipokuwa Mbunge wa Jimbo at least kupitia fedha za Mfuko wa Jimbo niliwasaidia jengo la upelelezi; nilipokuwa Mbunge wa Vijana, niliwapa mabati katika kujenga bwalo lao, tangu nilipofanya mimi kimya! Please, naomba Wizara iboreshe kile kituo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halafu na mahabusu, uzuri nami nililala pale, kwa Mkoa wa Mara labda kama sijalala mahabusu ya Serengeti. Mahabusu ile ni ndogo na mbaya yaani haina hadhi, inawezekana mahabusu hiyo watu 10 ikawa ni shida, hewa hakuna. Please, tunaomba pia Wizara ikarabati mahabusu ya Bunda.

Mheshimiwa Spika, tunaomba kile Kituo kiendane na hadhi ya wilaya, Wizara ipeleke na magari. Hivi leo hii akitokea mwizi Nyamswa, kukitokea uhalifu Mwibara, mafuta yenyewe shida, katika Wilaya yetu ya Bunda ambayo inaunganisha majimbo hayo matatu kama nilivyosema.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nizungumzie gereza la Jimbo la Bunda Mjini. Nilipokuwa Mbunge niliwakarabatia mahabusu moja, ikawapelekea na tv pale, ile mahabusu inatia aibu, nyumba za magereza Bunda Mjini ni shida.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na mradi umeanza tangu nilipochangia kidogo leo nyumba zipo kwenye lenta. Mpaka sasa hivi bado kuna shida kubwa mahabusu ile ya gereza la Bunda pale ni shida, lakini hata dawa kwenye Gereza la Bunda hakuna. Mdogo wangu kwenye uchaguzi alikamatwa, ilikuwa anaandika dawa ndiyo nampelekea. Je, wafungwa wengine wanakuwaje wasiokuwa na ndugu na wanatoka kwenye maeneo mbalimbali? (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, jambo lingine mlipe madeni ya polisi ya kuhamisha na mnapowapeleka kozi muwalipe kama watu wengine sio mnawakata kwenye mishahara yao wakati mnaenda kuwaongezea ujuzi. Ni aibu. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa dakika chache, nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natoka eneo la watu wanaofuga na wanaovua. Mheshimiwa Waziri, uncle, Halmashauri ya Bunda unaijua, wanafuga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ulega Halmashauri ya Bunda unajua wanavua, lakini Wizara hii hamjatuendea haki zaidi ya miaka mitatu mfufulizo tumekuwa tukiomba majosho, tumekuwa tukiomba mtukarabatie na kutujengea uzio kwenye minada, tumekuwa tukiomba machinjia kwa sababu lililopo ni la mwaka 1979 Mheshimiwa Ester Bulaya sijazaliwa. Lakini Mheshimiwa Ulega umejibu swali hapa maswali yangu ya kuomba vikundi vya uvuvi, Kikundi cha Wauza Samaki Bunda Mjini, Kikundi cha Ushirika cha Uvuvi cha Nyatwali vipatiwe mikopo; wameitikia wito wa Serikali wa kuvua kisasa, hivyo vifaa vya kisasa hawana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana sasa Mheshimiwa Waziri sisi tunauhitaji wa majosho Matano, Halmashauri ya Mji wa Bunda ina Kata 14, Kata saba ziko vijijini huko wanafuga. Tulikuwa tumeomba majosho Matano na ninajua kwenye fedha za majosho mnazo; Anko naomba hata mawili kwa mwaka huu wa fedha mahitaji yapo kwenye Kata ya Kunzugu, Mchalo, Kabasa, Waliku na Guta. Tunaomba walau kwa kuanzia mwaka huu wa fedha mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri unajua sisi Bunda tuna minada mitatu, lakini tunaomba walau kwenye minada miwili wa Bitalaguru Kata ya Kabasa na wa Kinyambwiga Kata ya Kunzugu. Halmashauri iliomba Milioni 257 kwa ajili ya hii minada na tukikarabatiwa tukaweka na uzio; mosi itasaidia utoroshaji wa mifugo lakini vilevile tutachangia hii Halmashauri mpya ya Bunda ili iweze kukusanya mapato na kufanya maendeleo yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri tulikuwa tunaomba machinjio na tayari tulishakuwa tumeomba milioni 150 kupitia mradi wa TACTIC bado hatujapata. Tunaomba machinjio, lile lililopo ni la mwaka 1979 wala Bulaya sijazaliwa, nimezaliwa, nimekuwa Mbunge, tunaomba machinjio mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ulega, umenijibu maswali zaidi ya mara tano kuahidi vikundi, leo hapa sema neno; vikundi vyangu vya wavuvi na vinanisikia sasa hivi vinahitaji fedha waweze kuvua kisasa na waweze kujiendeleza kimaisha. Amesema Mheshimiwa Tunza, hii sekta ya uvuvi mnaona kama ya watu maskini maskini hapana wawezesheni ili na wenyewe kama watanzania wengine. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia ya Wizara hii muhimu ambayo inatesa sana wanawake kwa kutembea umbali mrefu kutafuta maji na Mheshimiwa Rais amesema hilo jambo la maji ni kitu chake cha moyoni kwa sababu anajua wanawake wa nchi hii wanateseka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kuzungumzia tatizo la upotevu wa maji. Tatizo hili limekuwa sugu tangu nimeingia katika Bunge hili mwaka 2010 tunazungumzia changamoto ya upotevu wa maji kwenye mamlaka zetu. Nitoe mfano kwenye mamlaka 23, mamlaka 21bado zina changamoto ya upotevu wa maji kupita kiasi. Kwa miaka miwili tu kwa mfano mwaka wa fedha wa 2019/ 2020 kutokana na upotevu wa maji Serikali imepata hasara ya billioni 177. Mwaka 2081/2019 kutokana na tatizo hili la upotevu wa maji Serikali ilipata hasara ya bilioni 155. Sasa kwenye miaka miwili tumepoteza bilioni 332 ambazo Waheshimiwa Wabunge tutafakari, ingetengeneza miradi mingapi katika majimbo yetu, au tungechimba visima vingapi katika majimbo yetu na kumtua mwanamke ndoo kichwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine tunapoyasema haya, tunataka tatizo hili liishe na tunajuaje kuna upotevu wa maji? Ni baada ya kukokotoa maji yanayozalishwa na yanayomfikia mteja. Tatizo hili sugu kwa nini tunakubali kupoteza pesa za walipa kodi, kwa uzembe, kwa kutokuwa na ufanisi wa kuhakikisha miundombinu ya maji inakuwa salama na kuziba mianya ya watu kujiunganishia maji kiholela.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati haya yanaendelea, kwa mujibu wa Kanuni ya 6 ya mwaka 2013 ya Usambazaji Maji, Serikali inapaswa kupeleka ruzuku kwenye mamlaka ambazo zimefuzu, ziko Daraja A, B na C. Kwa mwaka 2019, Serikali imeshindwa kupeleka bilioni 856 katika mamlaka 10. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hizi mamlaka zitawezaje kujiendesha? Zinatakiwa zijiendeshe, zinatakiwa ziendelee na ukarabati wa miundombinu ya maji, na hizi halmashauri, ikiwepo na kwako Mbeya. Sasa haya mambo hatuwezi kuyavumilia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kweli huku tunashindwa kuminya, huku tunashindwa kuhakikisha tunatengeneza miundombinu mizuri ya maji, huku hatupeleki pesa kwenye mamlaka ziweze kujiendesha na kukarabati hii miundombinu ya maji halafu tunataka kumtua ndoo mwanamke kichwani. Kwa miujiza? Kwa mambo haya?

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na tatizo la kutokukusanya madeni kwenye mamlaka ya maji; bilioni 148 ziko nje! Lakini mbaya zaidi, Serikali inadaiwa bilioni 64 katika mamlaka zake. Lipeni madeni ili hii Wizara iweze kuweka mipango yake mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, madeni mengine, bilioni 83 ni kwenye viwanda na wateja wa kawaida. Tuna changamoto nyingi za miundombinu, tuna changamoto za kuhakikisha tunamaliza miradi kwa wakati, lakini bado Wizara hii imekuwa na changamoto kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo linguine Serikali kutolipa wakandarasi kwa wakati na kufanya riba ziongezeke; kwa mfano kuna ujenzi wa jengo la Wizara ambalo linagharimu bilioni 44. Lakini wameacha kulipa kwa wakati, riba imetoka kuanzia milioni 99 mpaka bilioni 4.9; shame! Hizi pesa mngekuwa mnalipa kwa wakati zingeenda kutengeneza miradi mingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa mtambo wa kusambaza maji Mradi wa Ruvu Chini, ambao Serikali inadaiwa bilioni 17 na Mchina, wameshindwa kulipa riba ni bilioni 3.9. Hivi kama mngelipa kwa wakati hizi pesa zingine zingeenda kukamilisha miradi mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kuna miradi sita Dar es Salaam, Moshi na Arusha imeshindwa kuendelea kwa miaka mitatu mfululizo kwasababu tu Serikali imeshindwa kupeleka bilioni mbili. Na huo mradi mpaka sasa hivi wamelipa bilioni 16, mradi una gharama ya bilioni 18. Mnalipa riba huku kwa uzembe wa kutokupeleka pesa kwa wakati, mnaacha miradi mingine ambayo inatakiwa ikamilike kwa wakati inashindwa kukamilika. Haya mambo ndiyo yanafanya Wizara hii ishindwe kutimiza wajibu wake na kuhakikisha mwanamke anatuliwa ndoo kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, hebu tujiulize hizi tathmini ambazo tunapewa kwamba upatikanaji maji vijijini maybe ni asilimia sabini na. nilikuwa nimepitia ripoti; EWURA inasema Mkuranga, Kisarawe, Chalinze, upatikanaji wa maji ni asilimia 96, lakini CAG amekwenda kuchunguza, upatikanaji wa maji ni asilimia 53.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, takwimu tunazopewa na Wizara na changamoto ya kutokamilika miradi na upotevu wa maji, inawezekana kabisa upatikanaji wa maji katika nchi yetu haufiki hata asilimia 50. Kwa hiyo, haya ni mambo ya msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa moja ya miradi iliyokaa muda mrefu ni pamoja na Mradi wa Maji wa Bunda unaotoka Ziwa Victoria. Biashara ya chujio tumeisikia sana, biashara ya usambazaji wa mabomba kwenye kata saba tumezisikia sana. Sasa tunataka kata 14 za Mji wa Bunda zipate maji; hilo ndilo nimetaka kulisisitiza. Zibeni mianya ya upotevu maji, pesa zinapotea.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wewe unasema wakikuzingua utawazingua, na sisi Wabunge humu ukituzingua maji hayatoki katika maeneo yetu na sisi tutakuzingua kabla Rais hajakuzingua. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwanza na mimi nikiri ni mwanahabari, nilikuwa newsroom takriban miaka sita magazeti ya Uhuru, Mzalendo na burudani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona watu wengi wamejikita katika michezo lakini pia Mheshimiwa Waziri waandishi wako wa habari wanalipwa vibaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utakubaliana na mimi na Waheshimiwa Wabunge waandishi wa habari wamekuwa wakifanyakazi kubwa sana na Taifa letu linawategemea waandishi wa habari kuielimisha jamii, lakini waandishi hawa wamekuwa na maslahi madogo sana, nani waandishi wa vyombo vya habari vyote vya Serikali na vyombo vya habari binafsi, siyo walioajiriwa tu mishahara yao midogo haiongezwi, hata correspondent journalist na wenyewe wanalipwa vibaya sana hapo nimezungumzia correspondent kwenye print media, sijazungumzia kwenye electronic media/ watangazaji nimezungumzia tu kwneye magazeti. Lakini wote wanalipwa vibaya sana na hawana watu wa kuwasemea.

Mheshimiwa Spika, sisi wanahabari kazi yetu ni kusemea wengine, lakini Bunge hili linapaswa kuwasemea waandishi wa habari wanatumia kalamu zao, wanatumia midomo yao kuhakikisha wananchi wanajua taarifa mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri na Mheshimwia Waziri wa Sera dada yangu pale Jenista baadhi ya vyombo vya habari havipeleki michango. Kwa hiyo, hatma ya waandishi wa Habari baada ya kumaliza kazi zao haieleweki nimekutana tu na baadhi ya wanahabari hapo wachache nje na wenyewe imebidi waanze kufuatilia kama michango yao inaenda, michango yao haiendi kwenye mifuko ya hifadhi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri mbali ya maslahi madogo kile wanachokatwa hakipelekwi, hilo nalo naomba ulifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri tabia ya kufungia fungia vyombo vya habari, tukubali/tukatae vyombo vya habari ni CAG mwingine, tusitake tu kutolewa habari za kufurahisha, lazima tukubali na kukosolewa zote ni habari za kujenga Taifa letu. Kwa mfano unakuta unafanyiwa interview mwandishi wa habari anakwambia Ester usiende huko tutafungiwa sasa unafungiwaje wazo nililolitoa mimi? (Makofi)

Kwa hiyo, kuna shida na ukweli soko la magazeti limekufa, sasa hivi hamna mtu ambaye wengi hawanunui magazeti kwa sababu anaona habari zile zile, habari za uchunguzi saa hivi zimepungua makala za uchunguzi zimepungua hebu hata ukienda kwenye mijadala angalia tathmini mbalimbali zinapotolewa watu wanatoa kwa hofu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hatusemi kwamba hakuna uhuru usiokuwa na mipaka, lakini tukiwahakikishia hawa waandishi wetu wa habari wafanyekazi zao kwa weledi hata kama wanapotukosoa magazeti haya hayafungiwi fungiwi hovyo, Mheshimiwa Waziri ukifungia gazeti moja ina maana umesimamisha zaidi ya familia 50; zaidi ya wafanyakazi 50 hawana ajira ina maana watoto hawaendi shule unawaweka hizo familia katika hali ngumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano tuzungumzie faini imekuwa kama chanzo cha mapato, watu walikuwa wanazungumzia upande wa michezo, hata huku kwenye magazeti, kwenye vyombo vya habari kuna shida, unamtoza mtu faini kubwa mtoze faini kidogo ajirekebishe, lakini siyo faini ikiwa chanzo cha mapato.

Sasa natolea tu mfano mlifungia Wasafi pale Babu Tale Mbunge anajua alivyofanya mpaka Wasafi ikafunguliwa, lakini je, hizi media zingine ambazo hazina watetezi? (Makofi)

T A A R I F A

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, Taarifa. (Kicheko)

SPIKA: Taarifa Mheshimiwa Babu Tale, declare interest.

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, dada yangu Ester sijafanya chochote ni utaratibu umefanywa na Serikali ndiyo maana tumefunguliwa, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Pokea hiyo taarifa Mheshimiwa Ester Bulaya.

MHE. ESTER A. BULAYA: Nimetolea mfano lakini anajua tulipokuwa tunakunywa canteen alisemaje.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema hizi faini zisiwe chanzo cha mapato mnapofungia gazeti moja mbali ya kumuathiri yule mwenye chombo, lakini mnawaathiri hawa waandishi wengine ambao mbali tu ya maslahi yao madogo, lakini pia unamfanya sasa anakosa kabisa kazi, anashindwa kuendeleza maisha yake. (Makofi)

Kwa hiyo nilikuwa naomba maslahi ya waandishi wa Habari tabia ya kufungia fungia vyombo hebu acha waandishi wa habari wafanye kazi kwa uhuru, tukosolewe, tujenge taifa letu, tusipongezwe tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia mmezungumzia hapa mpira, mmoja tu ndiyo amezungumzia timu ya wanawake, tena amegusa tu, hapa mnapozungumzia uwekezaji kwenye mpira wa miguu timu ya mpira wa miguu ya wanawake imekuwa kama mtoto yatima kwenye Taifa hili mbali ya kufanya vizuri timu ya Taifa ya Wanawake imekuwa ikichangiwa changiwa, aibu. (Makofi)

Lakini Mheshimiwa Waziri kwenye kurudisha michezo mashuleni hakuna programu ya timu ya mpira wa miguu ya wanawake hivi kweli ndiyo tunataka timu zetu zikashindane na Brazil, tukashindane na Senegal ambazo zinaenda ku- compete kwenye kombe la dunia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nitajikita katika kusisitiza umakini, usimamizi kwenye mikataba yetu kwa maslahi ya Taifa letu, hatuhitaji kujikwaa tena, lakini viporo tulivyoviacha lazima tuvifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe unajua mwaka 1997 Kampuni ya SONGAS ilianzishwa kama kampuni binafsi ambapo Serikali tulikuwa tuna hisa ya asilimia 40 na kampuni hii ilikuwa inafua umeme kutoka katika visima vya gas vya Songosongo. Sasa tunajua kwa nini Serikali iliamua kuingia ubia ni kutokana na tatizo kubwa la umeme ambalo iliikumba Taifa letu miaka ya 1990 mpaka 2000.

Mheshimiwa Spika, lakini kutokana na kusuasua na sintofahamu kutokea kutokana na uhalali wa hisa na mali za Serikali katika uwekezaji huu. Bunge lako Tukufu kupitia kamati inayohusiana na masuala ya nishati mwaka 2008 ilitoa taarifa kwamba mradi huu hauinufainishi Taifa letu, Serikali yetu inapunjwa na ikapelekea CAG kufanya uchunguzi. Moja ya mambo yaliyobainika ni kwamba mbali ya uwekezaji wa Serikali ya Tanzania wa asilimia 40 TANESCO ilihamisha mali na madeni kwenda kwenye kampuni ya SONGAS. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mali ambazo zinazohamishika zilikuwa na thamani ya dola za Kimarekani milioni moja, lakini pia mali zingine ni sehemu ya Ubungo Complex, mali zingine ni sehemu ya ardhi iliyokuwa inajengwa bomba la gas kupeleka kwenye Kiwanda cha Saruji Wazo. Lakini vilevile makubaliano yalikuwa yanasema SONGAS ilipe deni la mkopo lenye thamani ya dola za Kimarekani milioni 45.88 hadi tunapozungumza leo SONGAS hawakuamisha lile deni, zile pesa, lile deni linalipwa na TANESCO kupitia capacity charge kwenye ankara ya kila mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na hii CAG amesema kwa sababu TANESCO inaendelea kulipa lile deni wenyewe Serikali yetu ingeongeza thamani kwenye mradi na tungekuwa tuna hisa, lakini mpaka tunavyozungumza hili halijafanyika, mbali na kamati yako, Kamati ya Bunge inaisimamia Serikali kutoa maoni mbali na CAG tunapata kigugumizi wapi kulinda mali ya nchi yetu na mkataba unaturuhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kipindi hichohicho tuliingia mkataba na makampuni 936 katika kuhakikisha tunazalisha umeme wa dharura na makampuni yale uchunguzi ulivyofanyika ukaonyesha kabisa yalikuwa na gharama kubwa mpaka tunavyozungumza, mpaka 2018 kutokana na mikataba ile ya makampuni yale 936 TANESCO imekuwa na deni la bilioni 938. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini cha kushangaza kati ya makampuni 936 yaliyofanyiwa uhakiki ni makampuni 23 ambayo yenye thamani ya deni ya bilioni 643 hivi tunavyozungumza IPTL yenyewe imeshindwa kuthibitisha deni la bilioni 1.2 hivi tunavyozungumza makampuni 913 yameshindwa kuthibitisha deni ya bilioni 291, tujiulize kama Taifa tuna wanasheria, tujiulize kama Taifa hata kama tunapata crisis lazima tuwe makini katika kuingia mikataba, tuwe makini katika kuhakikisha mbali na kutatua tatizo tusiingie gharama kubwa hizi pesa zingeenda kumaliza miradi ya umeme vijijini, hizi pesa inawezekana tungepeleka katika miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kaka yangu Dkt. Kalemani nenda kamalize haya madudu yanatia aibu na inafanya TANESCO lishindwe kujiendesha, lakini tukija kwenye madeni bado sijazungumzia deni la TPDC la bilioni 246, Mheshimiwa Dkt. Kalemani unajua, hili deni tena la TPDC hili deni CAG amesema shirika letu linaweza likaporwa mali na Benki ya Exim ya China kwa kushindwa kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini wakati hii TPDC ni shirika la Serikali, Serikali wenyewe mnadaiwa, mnadaiwa na TANESCO bilioni 258, ili kulikomboa shirika letu mngeweza tu kwenye lile deni mnalodaiwa mngewalipia hawa TPDC hiyo bilioni 240 na, bilioni 9 inayobaki mngewapa TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kwenye uzembe wa kusimamia mikataba hata kama inatulinda. Mwaka 2004 Serikali iliingia mkataba na Kampuni ya PANGEA kwa ajili ya kutengeneza miundombinu ya umeme kwenye mgodi wa Buzwagi. Kwenye makubaliano ya ule mkataba ilikuwa kwanza wafungue benki ya pamoja kwa sababu kwenye makubaliano TANGEA walikuwa wanakata dola 5000 mpaka 3500 katika kila nusu saa ya ankara ya mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ninavyozungumza mpaka sasa hivi na yale makubaliano ili zile pesa ziende TANESCO, hivi tunavyozungumza na lengo lake lilikuwa kufanya miundombinu ikitokea hitilafu hivi tunavyozungumza takribani miaka kumi benki ya pamoja haijafunguliwa zile pesa zilikuwa zinaingia kwenye akaunti ya PANGEA na TANESCO ilikuwa inafanya ukarabati kupitia pesa zake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunavyozungumza bilioni kumi TANESCO haijalipwa aibu na hii tabia ya kutosimamia makubaliano ya pesa zetu wenyewe mikataba tunayoingia tunapata kigugumizi gani tunawaogopa wawekezaji wakati mikataba inatu- favor haya hata mikataba yetu wenyewe Mheshimiwa Waziri unajua TANESCO haijaingia makubaliano ikaenda kufanya ukarabati wa Mkongo wa Taifa na mpaka sasa hivi inaidai Wizara ya Mawasiliano bilioni nane hakuna mkataba na mpaka juni 2020 CAG anasisitiza ingieni mikataba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri lazima tufanye uchunguzi kwenye mitambo yetu ya kuzalisha umeme. Mtambo wa Kinyerezi I na Kinyerezi II ilijiwekea malengo ya kuzalisha Megawatt 398, lakini hivi tunavyozungumza malengo hayajatimia wamezalisha Megawatt 290, nenda kule Mwanza - Nyakato najua una mradi kule ilikuwa izalishe Megawatt 63, lakini wamezalisha Megawatt 36 hiyo ni miradi miwili ukijumlisha hapo ni Megawatt 155 zimepotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na hii yote wanasema ni tatizo la mitambo, huu wa Nyakato wanakwambia ni tatizo la, kulikuwa na matatizo kwenye mashine nne sasa hii ukienda haya matatizo ya kiufundi, matatizo ya kiufundi kwenye miradi mingi hivi ni Megawatt ngapi ambazo tunapoteza. Sasa Mheshimiwa Waziri haya ni mambo ya msingi ya kwenda kuyaangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ningependa kuzungumzia Mheshimiwa Waziri tatizo la mita kwenye mita kuu ambazo linasoma ni namna gani umeme wetu unavyozalishwa ni kiwango gani unapotea. Najua mlinunua mita 666, lakini mita zinazosoma ni mita 336 hii inachangia kutojua umeme unaozalishwa ni kiasi gani unapotea, lakini vile vile hili tatizo linatuletea hasara na inaongeza gharama ya uendeshaji.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Liganga na Mchuchuma limeongelewa tangu Bunge la Nane, tuko Bunge la Kumi na Mbili. Waheshimiwa Wabunge wenzangu, kwa maslahi ya Taifa letu tusikubali tukakamilisha kipindi chetu cha Ubunge bila Mradi wa Liganga na Mchuchuma kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Viwanda na Biashara ilieleza vizuri, Kamati yetu tumeeleza vizuri, huu mradi ni wa muda mrefu, leo tunaambiwa kuna Kamati inaangalia ni namna gani labda waachane na Mwekezaji au kupitia mkataba mpya. Huyu Mwekezaji ameshindwa kuwekeza hana mtaji wa dola za Kimarekani bilioni 2.9, hana! Tunabembelezana naye kwa nini? Mpaka sasa hivi tunavyozungumza alitakiwa amalize kujenga kiwanda cha chuma, alitakiwa amalize kujenga miundombinu ya umeme, alitakiwa alipe fidia ya wananchi watakaopisha ule mradi, ameshindwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Madini ipo wazi Kifungu Na. 47(1), twendeni ukurasa wa 123 unasema wazi kwamba mtu akipewa leseni ya uchimbaji anatakiwa ndani ya miezi 18 awe ameshachimba na kuendeleza, niwaulize Waheshimiwa Wabunge wenzangu, ni miezi 18 mingapi imepita tangu Bunge la Nane? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu sijawa Mbunge enzi ya Mama Mary Nagu tunazungumza Liganga na Mchuchuma! Mungu atupe nini? Leo hii tunaagiza chuma nje wakati chuma kipo kimelala pale, bado tunafikiria kuendelea na Mwekezaji huyu, sheria zetu za nchi zinatulinda na kwenye taarifa yetu tumesema, lazima Serikali muwe makini na kuangalia mitaji ya wawekezaji wanaokuja kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tunazungumzia Kamati inaangalia! Tunamlinda nani? Hivi kweli kwenye uwekezaji mkubwa wa namna hii wenye maslahi ya Taifa letu hatujui uwezo wa mwekezaji? Zaidi ya miaka kumi inapita hana dola za Kimarekani bilioni 2.9! Wananchi kule wa Ludewa wamekaa wanashindwa kuendeleza maeneo yao. Tunaomba Bunge la Kumi na Mbili lisiingie kwenye historia zingine, twendeni tulitendee haki Taifa letu, twendeni tukaweke historia kwamba kulikuwa kuna Bunge la Kumi na Mbili lilifanya maamuzi ya kuhakikisha uchumi wa nchi yetu unakua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati yetu tumezungumzia kuhusiana na kampuni ya uagizaji wa matrekta, hii ilikuwa tangu Awamu ya Nne, matrekta 2400 kutoka Poland, tangu enzi za Waziri Mkuu Mheshimiwa Pinda. Hata hivyo, mpaka leo yamekuja matrekta 800, matrekta 1,774, mabilioni ya shilingi pesa za walipakodi hayajafika. Ni aibu nikisema hapa tumeuliza kwenye Kamati wanasema, eti Kampuni imefilisika, yaani imefilisika kabla haijamaliza kuleta matrekta yetu? Tuna uwezo gani wa kugundua uwezo wa watu tunaoingia nao mikataba? Yaani ameleta matrekta 800 kampuni imefilisika, matrekta ya Watanzania ambayo yangesaidia wakulima wa nchi hii 1,774 hayajaingia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge hili, Kamati yetu ya uwekezaji tuliopewa jukumu la kusimamia pesa za walipakodi katika uwekezaji vitu kama hivi hatutaruhusu. Tunaitaka Serikali ije na majibu ya kina, matrekta ya Watanzania 1774 yatakuja lini? Haituingii akilini, watu wameingia tenda, wamesaini mikataba baada ya kuleta matrekta 800, baadaye kampuni ikafilisika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la EPZ. Tulipiga kampeni sana na tukatoa maeneo mbalimbali, tukatenga maeneo ya uwekezaji, leo hii EPZ ingefanya vizuri tatizo la ajira nchi hii ingekuwa historia. Hivi ninavyoongea kati ya Kanda 15 ni Kanda tatu tu zimeweza kuwekezwa, Kanda 12 wananchi wametoa maeneo yao hawajalipwa fidia na tumeambiwa EPZA iko kwenye ukwasi, ni kwa sababu Serikali haipeleki pesa za kutosha kwa ajili ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wetu wamesimama hawaendelezi maeneo yao. Kwa nini tunatafuta ugomvi na wananchi? Kwa nini tusiende kuchukua maeneo tunayoweza kuwekeza? Kanda 12 wananchi wamechukuliwa maeneo yao uwekezaji haujaanza halafu tunaimba ajira kwa vijana wa nchi hii wakati tunajua ni maeneo gani tunaweza tukafanya vizuri na tatizo la ajira nchi hii likapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Mheshimiwa Vuma amezungumzia kwenye suala la uwekezaji, naomba nizungumzie ni namna gani Serikali hawalipi madeni, hawapeleki michango ya wanachama.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyozungumza ATCL tangu mwaka 2008 mpaka 2016 haijapeleka michango ya wanachama, inadaiwa bilioni 16 hawajapeleka PSSF. Hizi ni pesa za watumishi wa nchi hii, walikatwa kwa ajili ya maisha yao baada ya utumishi wa nchi yao wanayoipenda sana. Nimesikia habari kwamba hawajalipa hizo pesa eti wanafanya mazungumzo wasilipe riba, come on! Pesa za watu walizochanga, ile siyo benki, ni pesa za wafanyakazi wa nchi hii waadilifu, wamekatwa zaidi ya miaka kadhaa ili waweze kupata manufaa baada ya kustaafu. Hapa kuna watu wamestaafu hawajalipwa pesa zao kwa sababu michango haijapelekwa, bilioni 16! Kuna watu wamekufa, kuna watu bado wanaendelea na kazi kwa uadilifu na uaminifu lakini michango yao haijapelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilisema hili suala kwenye vyombo vya habari, nilisema hili suala kwenye maeneo mengine, tunaomba pesa za wastaafu ziende.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua kwamba tathmini ya Mifuko imefanywa na iko Serikalini huu mwezi wa Tisa hamtaki kusema status ya mifuko ikoje na nimepata taarifa mmeanza kupunguza madeni ya Mifuko…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hoja aliyoongea Mheshimiwa Lusinde ni ya msingi. Ni kweli mtaani hali mbaya, ni kweli jambo hili Serikali mnatakiwa mlichukulie kwa udharura wake. Mliotoka Mikoani mnajua na maeneo mengine mnajua hali siyo nzuri ya upandaji wa mafuta pamoja na bidhaa mbali mbali. Kwa hiyo, ni jambo la msingi wananchi wana hali mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Wabunge, kama wawakilishi wa wananchi kuna wajibu mkubwa wa kulitafakari kwa kina suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba nijielekeze ukurasa wa 44. Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema Serikali ina mpango wa kuagiza ndege zingine ili zifike 16. Ni jambo jema sana na hakuna mtu anayepinga ununuzi wa ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunazungumzia hapa, hivi tunaendaje kufufua Shirika la Ndege? Kununua ndege peke yake ni kulifufua? Hili shirika kuna mipango madhubuti ya uendeshaji wa kibiashara? Je, tumeweka mikakati ya kuhakikisha ufufuaji wake utaongeza Pato la Taifa na uchumi kwa Taifa letu? Hayo ni mambo ni mambo ya kujiuliza, lakini suala la ndege kila Mtanzania anaona umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, 2016 wakati Shirika la Ndege linafufuliwa kwa Bombadia mbili ilikuwa na mtaji hasi Shilingi Bilioni 146, leo ina mtaji hasi Shilingi Bilioni 240, ukilinganisha mtaji na madeni ya takriban Shilingi Bilioni 371 haviendani! Sasa sawa tunaleta ndege hali ya Shirika la Ndege ni mbaya na Mheshimiwa Rais pia alisema linatakiwa lifanyiwe utaratibu liweze kujiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaleta ndege na matokeo yake ni nini, shirika hatujalipa mtaji, hatujaliwekea mikakati ya kibiashara, tumenunua ndege hatujalipa madeni ya ndani na nje ya nchi, ndege zinakamatwa, Serikali walichofanya wakakabidhi ndege kwa wakala! Wakala ni wa Serikali haizuii ndege kukamatwa, bado ni mali ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi wakati wanakabidhi wakala wa ndege (TGFA) lengo kubwa lilikuwa moja tu ni kwamba ndege zikinunuliwa zisikamatwe na wakasahau yule ni wakala wa Serikali wala hakukuwa na mpango wa biashara, bado tu ndege zilikamatwa!

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongeza gharama za uendeshaji, tunaongezea mzigo ATCL bila sababu na sababu siyo kukwepa ndege zisikamatwe sababu hapa kumaliza tatizo ni kulipa madeni na kuliongezea shirika mtaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndiyo naifananisha wakati tunasema mifuko ya hifadhi ya jamii ina hali mbaya wakaona walete sheria waiunganishe badada ya kulipa madeni kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii, ndiyo kinachotokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna madeni ndani na nje ya nchi hatutaki ndege zikamatwe tukapeleka kwa wakala haikuzuia ndege zinakamatwa kwa sababu yule wakala bado ni wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hapa ni kuweka mikakati dhabiti ya uendeshaji wa shirika letu tulipe madeni ndani, nje ndege zetu ziruke, tuitangaze nchi yetu na huku uchumi ukue. Sasa hii taarifa ni ya Serikali yenyewe wanasema hata Serikali ilivyohamisha umiliki kwa wakala TGFA bado haijaleta ufanisi na gharama za uendeshaji zimepanda zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano unapozungumzia matengeno ya ndege ATCL wao wenyewe wanatengeneza ndege kwa gharama kubwa kwenye kukarabati injini kwenye karakana zao. Lakini hapohapo wanalazimika kutoa tozo kulipa tozo za ukarabati kwa wakala, siyo sawa! Imeshafika zaidi ya takribani Shilingi Bilioni 99 madeni juu ya ukarabati wa ndege kwa wakala lakini wao wenyewe pia matengenezo makubwa wanayafanya kupitia karakana zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kwenda hivi, shirika haliwezi likawa na tija, lazima tujitafakari na uzuri hatujachelewa ni shirika letu wote tunapenda kuona fahari ya ndege, tukae tujipange namna bora ya kuendesha shirika letu la ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano nikutolee mfano kwa miezi Minne ile ya COVID-19 ilivyopamba moto, ndege hazikusafiri, lakini kwenye tozo peke yake ililipwa Shilingi Bilioni 15 ndege hazikuruka, kwenye ukarabati Shilingi Milioni 17 ndege hazikuruka miezi minne, sasa tunajiuliza kwa nini, hivi vyote tunafanya kwa ajili ya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tusiokoe hizi pesa zikaenda kutekeleza miradi mingine tukapunguza hali ngumu kwa wananchi wetu. Kwa nini haya madeni hizi hasara ambazo zinatengenezwa ambazo sasa hivi zimeshafikia zaidi ya Shilingi Bilioni 130 tungeenda kumaliza ahadi ngapi zilizotolewa kwenye majibu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunaendelea kulazimisha mkataba kwa wakala ambao ndege zinajiendesha bila faidi, zinajiendesha kwa hasara ambazo hizo hasara tungeweza kupunguza tukaenda kumaliza matatizo ya maji kwenye majimbo yetu tukamkomboa kumtua mwanamke ndoo kichwani? Ni sisi tu wenyewe kupanga ni kuchagua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma pia ukurasa wa 39 wa Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema wameweza kulipa pesa za mifuko ya hifadhi ya jamii zaidi ya Shilingi Bilioni Mbili kutumia hati fungani, sawa na hii ni ile ya Pre-98 sasa mimi niulize hii tu mmetumia miaka 22 ya Pre-98 hizi. Je, mtahitaji miaka mingapi mlipe madeni ya fedha za mifuko ya hifadhi ya jamii pesa ya wastaafu ya kuanzia mwaka 1999 kwenda mbele mnahitaji miaka mingapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa hizi hela mnakuwa kama mnazichukuwa tu hamlipi kwa riba, lini mlikopa kwenye mabenki mkalipa bila riba? tukisema hizi pesa za wastaafu wetu mnazitumia ndivyo sivyo, ndiyo maana wanakaa zaidi ya miezi sita zaidi ya mwaka hawajalipwa viinua mgongo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana tu wakati napitia simu yangu nikapata meseji, wastaafu wazee wangu kwenye Maktaba Kuu ya Taifa hawajalipwa na pesa zingine ile ni Maktaba ya Serikali Mwajiri hajapeleka michango wamepunjwa kwenye kiinua mgongo chao, kwa nini tunafanya haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana pesa za wastaafu zisichukuliwe poa! siyo sawa hawa wametumikia nchi yao kwa jasho na damu, mmekaa na hela za watu miaka 22, leo hapa Waziri akasema tunalipa kwa hati fungani hizo nyingine mtatumia miaka mingapi mliochukuwa kwenda kuwekeza kwenye viwanda na bado havijalipa vinatengeneza hasara. Mmechukuwa mkaenda kuwekeza kwenye majengo ambayo hayafanyi kazi hayajalipa, mtatumia miaka mingapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je watumishi wa Taifa hili waelewe nini wanayoipenda nchi yao, hawavumilii hawana wa kuwasemea ndiyo sisi tunakuja kuwasemea na bado wanafanya kazi kwa sababu wanajua kufanya kazi kuilinda nchi yao ni jukumu la kila Mtanzania, tuwatie motisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyakazi hatujawaongeze mishahara hatujawapandishia madaraja na bado pesa zao za hatma ya uzeeni hatujui zinafanya nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nami niungane alipoishia Kaka yangu Profesa Kitila Mkumbo, ni kweli kuna uhitaji mkubwa wa watumishi katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano tu kwenye Halmashauri ya Mji wa Bunda, tuna upungufu wa watumishi zaidi ya 900, Halmashauri moja tu ya Mji wa Bunda. Sasa ukija Watendaji wa Mitaa wapo 38 mahitaji ni 80, upungufu 50. Ukija Walimu wa Msingi, mahitaji ni Watumishi 1,252, Watumishi waliopo ni 738, pungufu ni 514. Ukija Maafisa Ugani Kilimo mahitaji ni Watumishi 48, Watumishi waliopo ni 34, pungufu 14. Watumishi wa Afya mahitaji ni Watumishi 402, Watumishi waliopo ni 184, pungufu ni 218.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa watalaam wa ujenzi mahitaji ya watumishi ni Tisa, waliopo ni watumishi watatu kwa Halmashauri moja tu ya Mji. Ukija Watendaji, Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Kata mahitaji ni 14 tunae Mmoja tu, Halmashauri ya Mji hiyo. Ukija Walimu wa Sayansi Na Hisabati; mahitaji 162 waliopo ni Walimu 88 na pungufu ni Walimu 74. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge hiyo ni Halmashauri moja Halmashauri ya Mji wa Bunda. Halmashauri imepata hati safi kwa uchache wa hao watumishi imagine mkitupa watumishi wa kutosha Mheshimiwa Jenista Dada Mkubwa mtupe wote 900 Mji wetu wa Bunda utakuwa kwenye hali gani? Tunahitaji watumishi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri, nimesoma ukurasa kuanzia 55 nimeusoma vizuri, 52 mpaka 55, ukurasa wa 105 mpaka ukurasa wa 108 nina maslahi hapa. Mheshimiwa Waziri amezungumzia kulipa Shilingi Bilioni 91 ya malimbikizo ya madeni ya Watumishi wa mishahara 65,000 malimbikizo ya madeni ya mishahara kwa watumishi 65,000 Shilingi Bilioni 91.

Mheshimiwa Spika, ukisoma ripoti ya CAG yaani hii mpya latest Machi, 2022, watumishi wanawadai Shilingi Bilioni 430 ya malimbikizo ya muda mrefu, siyo mishahara peke yake kuna malimbikizo ya mishahara ya watumishi wapya, kuna malimbikizo ya watu waliopandishwa madaraja na posho za watumishi, lakini hapa mmelipa Shilingi Bilioni 91 peke yake, bado mnadaiwa Shilingi Bilioni 399 mnazilipa lini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona hapa mmetenga Bilioni 103, kutenga ni jambo lingine kulipa jambo lingine na hata hili mkifanikisha kulipa bado mtakuwa mnadaiwa Shilingi Bilioni 236. Je, mtazilipa lini? Siyo sawa Serikali kuendelea kudaiwa malimbikizo ya Watumishi ambayo ni haki yao ya msingi.

Mheshimiwa Spika, kwa mtindo huu ukiangalia unakuta mtumishi anaanza kuidai Serikali alipoajiriwa tu ana malimbikizo ya mshahara, haya akipandishwa madaraja bado lile daraja alilopandishwa haliendani na mshahara anaotakiwa kulipwa, bado ana malimbikizo. Haya, imefika tena kustaafu bado anaweza akaa miaka 20 hajalipwa kisa utaratibu wa mafao haujafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dada yangu Mheshimiwa Waziri naomba unisikilize hilo nimesema la madeni, bado wastaafu wetu wanacheleweshwa kulipwa mafao yao. Ukiuliza sababu ni kwamba majalada yao maandalizi ya mafao hayajafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mfano mpaka tunavyoongea kwenye taarifa mpya ya CAG majalada 571 hayajafanyiwa kazi, kuanzia mwaka wa kwanza mpaka wa 28. Mstaafu amestaafu waliokaa miaka mitatu ambao hawajalipwa ni 391. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kaanza kwenye stress za kucheleweshewa mshahara, kulundikiwa malimbizo anakutana nayo tena huku kwenye kulipwa kiinua mgongo chake, siyo sawa kwa watumishi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waliokaa miaka mitano hawajalipwa mafao yao baada ya kustaafu wako 59. Waliokaa Miaka Kumi ni Wastaafu 54. Miaka 20 wapo Wastaafu 17. Waliokaa miaka 15 ni Wastaafu 25. Waliokaa miaka 25 ni Wastaafu 18, Waliokaa miaka 28 ni Wastaafu Saba, jumla ni Wastaafu 571 ya wastaafu wa Taifa hili waliotumikia Taifa lao kwa jasho na damu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa huku hatuwapandishii mishahara, tukiwapandisha madaraja malimbikizo lukuki, tukiwaajiri malimbikizo lukuki, Serikali mnaanza kudaiwa na wafanyakazi wanapoajiriwa, wanapopandishwa madaraja na wanapostaafu hamuwalipi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri naomba sana tuwatende haki wafanyakazi na watumishi wa Taifa hili ambao wanatumikia Taifa hili kwa jasho na damu na hawalalamiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa kuna kipindi wamekaa miaka Mitano hawajapandishwa mishahara wapo tu wanalijenga Taifa lao. Sasa Mheshimiwa Waziri hapa nimelizungumzia bado taasisi zako kuna taasisi 15 na Mheshimiwa Spika nakupongeza, taasisi yako inapeleka michango wengine hampeleki. Nitolee mfano shirika la reli haijapeleka michango ya watumishi Shilingi Bilioni 99. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Maji ndiyo wamekuwa sugu maana hata penalty hawalipi wanadaiwa penalty huko Shilingi Milioni 441 hawajapeleka. TRA wakusanya mapato pelekeni michango ya wafanyakazi. Bodi ya Mikopo, Mfuko wa Bima, nitaje na wengine?

WABUNGE FULANI: Taja! (Makofi)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, pelekeni michango ya watumishi kwa mujibu wa Sheria ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, Serikali ndiyo wasimamizi lakini taasisi zenu zinaongoza kutopeleka michango na hii ina athari kwenye kiinua mgongo cha watumishi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine ninyi ndiyo mnachangia hii mifuko kufa, tuliwaomba hapa actuarial valuation hamjaleta, sasa CAG ameamua kufanya kwa mlango wa nyuma. Kwenye ripoti ya mwaka huu kwa mujibu wa Sheria ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya mwaka 2018 inasema mifuko walau iwe na ukwasi wa asilimia 40.

Mheshimiwa Spika, PSSSF, mfuko ambao ndiyo unaosaidia Watumishi wa Umma una ukwasi wa asilimia 22. Mlivyolipa kale kahela Shilingi Trilioni Mbili kwa hati fungani, kidogo ndiyo kamesaidia imefika asilimia 30 lakini bado ni chini ya sheria inavyotaka. Sasa nauliza na CAG amependekeza Shilingi Trilioni 2.45 iliyobaki mnailipa lini ili kuokoa huu Mfuko?

Mheshimiwa Spika, hii ni 399 bado ya madeni mengine. Sasa mkiangalia mzizi wote ninyi ndiyo mnatengeneza tatizo, ninyi ndiyo mnatupa ahadi hapa na bado hamtekelezi kwa wakati na bado wafanyakazi mfuko wao una hali mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi mnawezaje kupata guts za kuwahamasisha sekta binafsi wapeleki michango wakati ninyi wenyewe hampeleki michango? Ninyi wenyewe hamlipi madeni. Sasa huu ni mfuko wa wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu NSSF mna madeni sugu ya Shilingi Trilioni 1.5 Serikali hamjapeleka, Mheshimiwa Waziri naomba tuilinde hii mifuko tutimize wajibu wetu, tusaidie wafanyakazi wetu, please!

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi).
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Amiri Jeshi Mkuu wa Nchi yetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amekerekwa na ubadhilifu, mimi ni nani Ester Bulaya niuchekee? Kama Waziri Mkuu wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesikia kwenye ziara zake mbalimbali akikemea ubadhilifu mimi Ester Bulaya mwakilishi wa wananchi ni nani niuchekee na hasa jicho likiwa limefanya kazi yake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumsaidia hivyo hivyo Rais kwa kuisaidia Serikali iweze kuchukua hatua lazima tuonyeshe kwenye mapungufu hatua zichukuliwe nchi yetu isonge, maendeleo ya Taifa yaonekane kwa wananchi wake.

Mheshimwa Mwenyekiti, kwa utangulizi naanza. Kikokotoo Wafanyakazi bado wanalia, tusitengeneze mgomo baridi, hawa ndiyo wanaoenda kutekeleza miradi ya maendeleo, najua mnasikia, najua mmeona na najua mkiamua kulifanyia jambo mnaweza, bado asilimia 33 si haki yao, maisha magumu Wafanyakazi wanalia wanafanya kazi kwa kinyongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 14 wa Waziri Mkuu, hotuba yake ameisoma vizuri tu hapa, kuzungumzia miradi ya kimkakati na anazungumzia mradi wa Mkulazi ambao amesema upo asilimia 75, tunataka majibu ya kina hapa kuna fedha za Mifuko zimewekezwa. Je tathmini ya kina ilifanyika? Maana ripoti mbalimbali za CAG zimeonesha hapa pametengeneza hasara ya bilioni 11 sawa na asilimia 21 ya mtaji uliowekezwa, Mkulazi hapa. Moja ya sababu inasemekana kulikuwa kuna ucheleweshaji wa mashine. Sasa ukienda ya mwaka huu inasema hiyo mashine aliyepewa tenda ya kununua mtambo wa kutengenezea Kiwanda cha Sukari ni Wakala wa Barabara TANROADS, wapi na wapi! Kwa nini haikuwa TEMESA, kwanini haikuwa wakala wa kuagiza vifaa Serikalini, TANROADS, barabara wa sukari wapi na wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kuna fedha za Kimarekani takribani milioni 50.8 na inasemekana mbali ya kwamba na huu mkataba ambao Mkulazi hawajashiriki hata kuweka Saini, kila kitu walifanya TANROADS. Kuna nyongeza ya bilioni 11 na hatujui kwamba Mwanasheria Mkuu alithibitisha kwa mujibu wa Kanuni ya 59(1) cha manunuzi. Tunataka majibu ya kina, haya tunayasema kwa sababu tunataka hatua zichukuliwe, watu wasiichukulie Serikali poa, watu watimize wajibu wao, hizi ni fedha za wastaafu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni Mkulazi bado kiwanda cha Ngozi cha Kilimanjaro hasara Bilioni Nne, fedha za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii shilingi bilioni nne. Katika malengo yao hicho kiwanda kipya cha Kilimanjaro kilikuwa kimepanga kuzalisha jozi za viatu 1,200,000 wakazalisha 11,354, kilikuwa kimepanga kuzalisha jozi za sori za viatu 900,000 kikazalisha sifuri. Kilikuwa kimepanga kuzalisha bidhaa za ngozi 48,000 kikazalisha 224, kilikuwa kimepanga kuzalisha ajira 300 kikazalisha 79. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo hayajafikiwa usimamizi mbovu kwenye pesa za wastaafu zinazoenda kuwekezwa kwenye viwanda. Wakati haya yanafanyika bado mifuko iko hohehahe PSSF tena ripoti mpya ambayo tutaenda kushughulika nayo huko mwezi wa Agosti, PSSF imesema Mfuko ukwasi upo asilimia 22 kinyume na sheria cha asilimia 40. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nimesema na leo narudia, wakati hizi pesa zinaendelea Trilioni 1.5 pesa za muda mrefu hamjalipa kwenye Mifuko tuliahidiwa na Waziri wa Fedha akalipa kwa Hati Fungani nyingine hamjatoa, wakati haya wanaendelea Mfuko wa PSSF umelipa bilioni 767 pesa za Wastaafu, kiinua mgongo chao zaidi ya mapato waliyonayo kuna mwaka walienda kukopa kwenye maeneo mengine, kiasi walicholipa ni kingi kulingana na mapato ya michango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati haya yanaendelea kuna mashirika manne hayajapeleka michango takribani bilioni 129 kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, wakati haya yanaendelea kuna Mamlaka ya Serikali za Mitaa 133 hazijapeleka takribani bilioni 119 maslahi ya mishahara na posho za wafanyakazi hazijalipwa. Wakati haya yanaendelea kuna mashirika nane hayajalipa malimbikizo ya mishahara ya watumishi na madeni mbalimbali takribani bilioni 5.8, bilioni 2.2 ni malimbikizo ya mishahara. Wakati haya yanaendelea kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa kuna Mamlaka 76 hazilijalipa milioni 309 za mizigo za wastaafu 223. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayasema haya kwa sababu tunataka nchi yetu iende, haya mambo Bunge tumekuwa tukiyaongea mara kwa mara na Serikali haifuati maagizo ya Bunge. Niwaambie tu kwenye maagizo ya Bunge 892 ya Kamati ya LAAC yaliyofanyiwa kazi ni asilimia 26 tu, yamefanyiwa kazi maagizo 228. Kwa nini Hoja za Ukaguzi zisijirudierudie? Hapo kuna maagizo 159 ya Bunge lako Tukufu hayajafanyiwa kazi takribani miaka 10. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge lazima tutimize wajibu wetu, tuibane Serikali itimize wajibu wake, tumsaidie Mheshimiwa Rais ameonesha makasiriko yake ya kukerwa, lazima kama Wabunge, kama Taifa tusimame imara, hatumtafuti mtu hapa, tunataka tuwatendee haki Watanzania fedha zao ziende kwenye miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haya Maagizo ya Bunge hayafanyiwi kazi, kwa nini Wakurugezi kule wasifanye mambo wanayojitakia kwenye Halmashauri? Kwa nini pesa za vikundi zisipigwe takribani shilingi bilioni 88? Kwa nini asilimia 40 za kisheria zinazopaswa zikusanywe na Halmashauri hazikusanywi? Kwa sababu Bunge tunatoa maagizo, hamsikilizi. Tunaomba haya maagizo yakafanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua Mheshimiwa Waziri Mkuu ni mnyenyekevu, tunaomba watumishi watimize wajibu wao. Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, madeni yalipwe. Watumishi pesa zao kwa mujibu ya sheria, michango ipelekwe. Kwenye uwekezaji kuwe na tija. Ifanyike tathmini ya kina ili hizi pesa za hawa watumishi wa umma ambao ni wastaafu watarajiwa, huku wanapigana na stress za kikokotoo, huku pesa zao hawajui huko zilikoenda zitarudi kiasi gani? Please! Naomba sana tuwatendee haki Watanzania, tuwatendee haki watumishi wa Taifa hili. Haya tunayopanga, wao ndio wanaenda kutekeleza, hawataenda kutekeleza wakiwa na stress, hawajui hatima yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi namimi niweze kuchangia Wizara hii ya Viwanda na Biashara.

Kwanza Mheshimiwa Waziri ukija kuhitimisha hoja yako sisi wananchi wa Mkoa wa Mara tunahitaji utujibu kuhusiana na viwanda vyetu vilivyokufa pale Musoma. Kiwanda cha nguo, kiwanda cha kusindika samaki na kiwanda cha maziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, viwanda hivi vilikuwa vina mchango mkubwa sana katika kutengeneza ajira katika Mkoa wa Mara. Mheshimiwa Waziri kuna kipindi mlihamasisha sana wananchi watenge maeneo kwa ajili ya ukanda wa uwekezaji. Eneo moja wapo watu walilolitenga na wakalipwa fidia ingawa wengine wakadhulumiwa ni Wilaya ya Bunda. Ni zaidi ya miaka 10 sasa hivi hakuna hata kiwanda kilichowekezwa. Ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha maeneo yale yaliyotengwa kwa ajili ya uwekezaji yanawekezwa ili wananchi wa pale waweze kupata faida, iweze kutengenzwa ajira kutokana na malighafi zinazopatikana maeneo husika? Ni muda mrefu sana tunahitaji majibu ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mimi ningependa Mheshimiwa Waziri ukija hapa uje utueleweshe sisi Wabunge kuhusiana na hii issue ya Twiga Cement, Tanga Cement; yaani bado hatujaielewa sana. Tunaomba ukija uchukue muda mwingi sana kulielezea hili jambo ili sintofahamu ziondoke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa najaribu kuuliza katika hili jambo, kwamba maslahi ya taifa yakoje, nimejiuliza sana. Sasa, kuna Tanga Cement anataka kuuza sehemu ya share kwa sababu kashindwa kuendesha, kwa sababu ameshindwa kulipa kodi kwa zaidi ya miaka saba. Si kwa kupenda yeye bali ni kwa sababu hawezi tena kujiendesha. Kuna athari ya zaidi ya wanfanyakazi 3,000 kupoteza ajira hapo. Sasa yeye pamoja na wabia wenzie, maana hili la kwao, wamehamia kuuza sehemu ya share kwa Twiga ambaye yeye anataka ku-invest dola milioni 400 sawa na shilingi bilioni 930. Yeye ndiyo ameona huyu sasa anataka kutupa hizi fedha. Wamekubaliana wao, sasa sijui kizungumkuti kiko wapi.

Mheshimiwa Spika, sasa kama kuna mwingine alikuwa na fedha nyingi tulitarajia angewafuata Tanga Cement wakubaliane, kwa sababu hapa ni biashara huru. Wao wenyewe wana mamlaka ya kuchagua waende kwa nani, kwa namna gani wao wanaweza kuokoa eneo hili. Kwa hiyo tunahitaji tupewe maelezo ya kina lakini huyu ambaye anataka ku-invest hapa ni mlipakodi mzuri. Mwaka jana amelipa zaidi ya shilingi bilioni 80 lakini hapa Tanga Cement wamepata hasara zaidi ya shilingi bilioni 46, hawawezi kujiendesha, kizungumkuti kiko wapi hapa?

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nafanya uchunguzi wangu na nikapata taarifa; nimesoma Gazeti la Jamhuri la uchunguzi la tarehe 24 mwezi wa nne. Limesema, kwa sababu kulikuwa kuna hoja, ooh! huyu akimilikishwa kuna suala la ku-dominate soko. Sasa nikaambiwa Tume yenyewe ya Haki ya Ushindani ilifanya kikao na hawa wazalishaji 12 wa saruji, na wakasema kwamba sisi hatuna nongwa, hakuna suala hapa kwamba hawa wata- dominate soko kwa sababu mazingira ya sasa hivi yamebadilika, wapo watu ambao wana uwezo wa kuzalisha zaidi ya tani 1,000,000 ya cement.

Mheshimiwa Spika, hata kama sasa hivi Twiga anaongoza, Dangote akiamua kufungulia mitambo yake naye anaweza akaongoza vile vile. Huyu mwingine naye akiamua kuongeza uzalishaji naye anaweza akampita Dangote anaweza akampita Twiga, suala la dominant hapa liko wapi? Tunaomba utuelezee. Na nikaambiwa kati ya hao wazalishaji 12 kuna wengine hawakwenda. Hawakwenda kumbe kwa sababu hawazalishi. Sasa tunahitaji tupewe maelezo ya kina hapa tujue interest ya taifa iko wapi hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima tupewe maelezo ya kutosha; na mimi sitaki kuwa na upande na hizo siyo tabia zangu. Tunataka kujua interest ya taifa iko wapi? Mnufaika ni nani? Yaani kama wenyewe wazalishaji wamesema hakuna nongwa, tatizo linakuwa wapi?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri uje utuambie hapa tupate maelezo ya kina ili sintofahamu ziondoke. Maana hapa isije ikawa tunaingizwa kucheza ngoma ambazo hazituhusu, na hizi ngoma inawezekana ziemanzia kwenye Wizara yako huko huko kuna, makundi kwa sababu kuna interest za watu. Tunahitaji majibu sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ukija hapa hebu tueleze hili suala la ukomo wa asilimia 35 limekaaje. Hivi, kama mtu aliomba kwenye mazingira hayo ya kipindi hicho akakataliwa, hivi ni alpha na omega? Hana room ya kuomba tena? Waliokataa hawana room ya kukubali kwamba sasa hivi mazingira ya uwekezaji yamebadilika? Ikoje hii?

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri tunaposema tunavutia wawekezaji kuna wawekezaji ambao wameshaanza ku-invest. Tunajua mitaji yao, tunajua uwezo wao, tumewaona; hawa wanatakiwa walindwe. Nilikuwa nakumbuka kulikuwa kuna sarakasi moja hapa ya issue ya Dangote akataka kuondoka, kwa taarifa nilizonazo Serikali ikabidi mwende kumbembeleza ili abaki. Tunazungumzia hapa Liganga na Mchuchuma kuna muwekezaji amekaa pale muda mrefu, leo Serikali inabidi muende mkawalipe fidia ili muanze uzalishaji kwa sababu alikuwa hana capacity hiyo.

Mheshimiwa Spika, tunataka tuendeleze uwekezaji wa briefcase? Kama tutakuwa wakweli na tunaipenda nchi hii nyekundu iwe nyekundu, njano iwe njano, uweke historia. Mara mia uhukumiwe kwa kusema ukweli lakini siyo uhukumiwe kwa kupindisha mambo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kiukweli, kiroho safi, hata kama wengine hatupongezi hovyo hovyo, Mheshimiwa Aweso anafanya kazi na Naibu wake. Ni term yake ya kwanza humu Bungeni, lakini akikaa kwenye podium utadhani ni mzoefu zaidi. Pia nimpongeze Katibu Mkuu, nimpongeze na kaka yangu kijana wa Bunda, Naibu Katibu Mkuu, anatuwakilisha vyema wananchi wa Mkoa wa Mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Aweso sifa yake pekee ni unyenyekevu, hajavaa cheo. Mungu ambariki safari yake ya kumtua mwanamke ndoo kichwani itimie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kuchangia na nashukuru Waziri wa Fedha yupo hapa anisikilize. Hivi kwa nini Serikali na taasisi zao hawataki kulipa madeni ya maji wakati wanatumia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa aliwakumbusha Wabunge walipe madeni ya nyumba, leo tunawakumbusha wao wasitumie maji bure, walipe pesa za maji, ili mamlaka za maji kwenye maeneo yao hizi shida ndogondogo waweze kuzifanya. Hivi mbona hatuoni wakienda sheli nyie kukopa mafuta kwenda kufanya ziara? Au kwa sababu, Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na watendaji wake hawawezi kusimama hapa kuwadai madeni? Yaani wanatakiwa wadaiwe na wafanyakazi, wadaiwe, hata kulipa maji wanayotumia kwenye taasisi zao? Aah, I see? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naanza hapa kwa kutoa mfano, Tanga, Mamlaka ya Maji Tanga inadai taasisi za Serikali bilioni 2 na milioni 477, wanatumia tu. Kwa nini hawaendi shell kukopa? Kwa nini huku wanatumia maji hawalipi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naendelea, Masasi inadai taasisi za Serikali milioni 307 na hii mpaka ilitokea aibu, mamlaka ikataka kwenda kukata maji Hospitali ya Wilaya, walipe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naendelea, haya, taasisi mbalimbali DAWASA, inadai bilioni 9.0 hee! Miaka mingapi hii hawajalipa bili ya maji? Wananchi wanalipa bili ya maji, private sector wanalipa bili ya maji, kwa nini wao hawalipi bili ya maji? Walipe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naendelea, Newala wanadai milioni 33.7, Mamlaka ya Maji Tabora milioni 126, Sumbawanga milioni 122, Kigoma milioni 534, Mtwara bilioni 1.3, Nzega milioni 22. Hapa namtetea Mheshimiwa Bashe. Naendelea, Korogwe milioni 21; Mamlaka ya Ludewa milioni 17. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi mnataka hizi mamlaka zijiendesheje? Kwa nini mnamchelewesha Waziri wa Maji Mheshimiwa Aweso safari ya kumtua mwanamke ndoo kichwani? Hivi wananchi hawa wanafanya biashara kwa kipato kidogokidogo wanalipa bili ya maji, ninyi hamtaki kulipa bili ya maji. Wanachi wasipolipa wanakatiwa, Mheshimiwa Aweso, kwa nini usikate? Waende siku moja ofisini wakose hata maji ya kuosha vikombe vya kunywea chai. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Unipe taarifa ya Yanga kushinda, mengine siyataki. (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Ester Bulaya, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Waziri wa Fedha na Mipango.

TAARIFA

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge anayechangia, nimeona tangu mwanzo amesema na Waziri wa Fedha yuko hapo na kila anapochangia namuona ananiangalia.

Mheshimiwa Spika, ninataka nimpe taarifa kwamba nasi Wizara ya Fedha tunahimiza taasisi zote zinazotumia huduma zilipe. Zikishalipa wasitengeneze madeni mengine. Huu ndiyo msimamo wa Mheshimiwa Rais na ndicho ambacho tumekuwa tukisisitiza sisi tunaosimamia mafungu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninataka nimuunge mkono Mheshimiwa Mbunge na kwa kweli nitoe rai taasisi zinapotumia huduma wanatakiwa walipe na wasitengeneze madeni, hiyo ndiyo itakayochachua uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitaka nimpe taarifa tu maana yake nimeona ananiangalia kwelikweli. Ninaomba kutoa taarifa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ester Bulaya, badala ya kumuangalia Mheshimiwa Waziri kwa sababu unaongea na Spika mwangalie Spika ili usimtishe Mheshimiwa Waziri. Unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, mimi kwanza siipokei, lakini hapa nakuangalia wewe ambaye na wewe hutaki madeni.

Mheshimiwa Spika, hivi anaongea tu hela wamepeleka sasa, hao anaotaka walipe? Hela za bajeti tukipitisha hapa anapeleka zote kule? Lipeni madeni. Leo hapa tutataka mtuambie mtaanza kutenga shilingi ngapi ili mlipe madeni.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kunti jana alisema, machache tu ni shilingi bilioni 33 sasa unganisha nilizozisema mimi. Mnatumia maji bure tu. Siku moja Mheshimiwa Aweso nakwambia Kata washindwe hata kuosha vikombe vya kunywea kahawa ofisini, uone kama hawatalipa madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mwanangu nisikilize mama yako nina ombi na andika kabisa. Nashukuru Mradi wa Maji wa Bunda wa kutoka Nyabehu umefika Mjini, umeanza kusambazwa baadhi ya maeneo. Nawe uliukuta ukiwa na asilimia 40, mimi na wewe tumefikisha asilimia 99 kufika pale Mjini, ninachotaka Kata zote 14 za Halmashauri ya Mji wa Bunda Mjini zipate maji. Tunahitaji shilingi bilioni saba tuweze kuhakikisha tumeweka miundombinu ya maji katika Kata zote 14. Hivi leo maji yanayozalishwa zaidi ya asilimia 45 hayatumiki kwa sababu gani; hakuna miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Aweso, sasa nisikilize, kuna ujenzi pale wa tenki ambalo litakuwa na ujazo wa milioni tano, hapa zinahitajika bilioni tatu. Naomba huu mradi ukamilike, wananchi wa Bunda waweze kupata maji safi na salama. Kwa mfano, kueneza mtandao wa maji Kata ya Guta, ili kata nzima iweze kupata maji zinahitajika milioni 876. Kata ya Wariku, milioni 786, Sazila milioni 564, kwenda Kiwasi milioni 687. Sasa huku ukitaka kwenda Nyamatoke – Bukole milioni 987, sasa na kusogea huku Bunda DC milioni 456. Tunahitaji tusiwe na mradi tu ambao umefanya maji yaje mjini, tunahitaji maji kwenye Kata zote 14. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waliopo humu tangu 2010 wanajua huyu ni mtoto wangu niliyemlea, sasa amekua anataka kutembea kwenye Kata zote 14 wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Bunda wapate maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Aweso jambo lingine, Mamlaka ya Mji wa Bunda bado changa, hampeleki ruzuku. Unajua shida yake? Wanaongeza bili inakuwa kubwa kwa wananchi na wanalipa kwa sababu wanahitaji maji. Tuwapunguzie mzigo, tupeleke ruzuku waweze kujiendesha. Halafu ule mradi sasa usiwe laana, uwe una neema na bili ya maji iwe standard. Nimesema wananchi hapa wanalipa bili za maji, ambao hawataki kulipa ni huko Serikalini tu, tunaomba bili iwe fair, wananchi wameupokea mradi, mkikamilisha Kata 14 watalipa bili kwa wakati na hizo fedha wataweza ku-maintain maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, bomba kuu linalotoka katika ule mradi linamwaga maji, linavuja, kuna upotevu mkubwa wa maji, ukitoka huku Bunda Store mpaka kule Nyamakokoto maji yanamwagika sana. Tunaomba muangalie, hii inachangia upotevu mkubwa wa maji. Nendeni mkaangalie tatizo ni nini kwenye lile bomba. Naomba sana, ambalo pia linakwenda mpaka kule Kaswaka, naomba muangalie sana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, jambo lingine…

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Ahaa, ndiyo nilikuwa nashuka mambo ya Bunda. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie na ninachangia jioni ya leo huku Kaimu Waziri Mkuu Kapteni George Mkuchika akinisikiliza, Waziri Senior kabisa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kwa kuwa yeye ni Waziri Senior anajua migogoro ya ardhi katika nchi yetu ilivyokithiri, kwa hiyo naamini Kaimu Waziri Mkuu atamshauri Waziri husika na Naibu wake na hasa ukizingatia michango tangu asubuhi hii ya leo imeonesha ni namna gani migogoro ya ardhi katika nchi yetu bado haijapatiwa ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la Nyatwali tu leo hii. Suala la Nyatwali lilikuwepo tangu enzi ya Rais Awamu ya Nne Baba yangu Jakaya Mrisho Kikwete, akalisitisha kwa sababu hakutaka kuingia kwenye historia ya dhuluma ya wananchi wa Nyatwali. Suala la Nyatwali, Mungu amlaze mahali pema Hayati John Pombe Magufuli alilisitisha. Mmekuja Mheshimiwa Waziri mnataka kumuingiza Rais Awamu ya Sita aingie kwenye mgogoro na wananchi kwa sababu mnataka kumshauri vibaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili haliwezekani, wananchi wa Nyatwali waligoma kuhama kabisa, kabisa kwa sababu ya wasiwasi wa kudhulumiwa. Mkatumia nguvu kwenda kuwatisha, kipindi changu mimi niligoma na nikawaambia kuhama siyo issue, issue mnawahamisha kwa fidia ipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkumbuke eneo la Nyatwali ni lao wako pale zaidi ya miaka 700, leo kwa dhamira yao mnawatisha, mnawashurutisha, tena mpaka Viongozi wa CCM, viongozi wa vijiji, Diwani mnawaita Polisi kuwashurutisha wananchi wanyonge wale na ninyi mnasema ni Serikali sikivu. Kwa nini hamtaki kuwasikiliza wananchi wa Nyatwali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mnawalazimisha kuhama, sawa wamekubali, kweli nchi hii eneo la Nyatwali, eneo la lango kuu la kuingilia Mbuga ya Serengeti, eneo very prime, muende mkawalipe fidia ya shilingi 400 kwa square meter? Yaani mnataka kutuambia thamani ya ardhi kwenye Mbuga ya Serengeti, Nyatwali thamani yake ni ndogo kwa square meter kuliko Coca- cola, Coca-cola shilingi 500. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mnataka kutuambia wananchi wa Bunda Mjini, thamani ya ardhi kwenye lango kuu la kuingia Mbuga ya Serengeti, Mbuga namba moja inachukua tuzo kila siku, thamani yake kwa square meter ni shilingi 400, Coca-Cola shilingi 500, chipsi kavu buku (shilingi 1,000)? Hatuelewi watu wa Mara. Watu wa Mara hatutawaelewa na mnatujua. Hatuhitaji migogoro na ninyi, tunahitaji haki yetu. Hivi leo unampa shilingi 400 kwa square meter, jirani Kata ya Bariri viwanja vinapimwa square meter ni shilingi 3,000. Mnataka kuwatoa watu 13,000 mkawafukarishe siyo sawa! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa namsikia Mbunge anayetoka kwenye makaa ya mawe kule anashukuru watu wake wanalipwa, nataka nijue, hivi kule nako mnawalipa shilingi 400? Watu wa Mara tumewakosea nini? Shilingi 400! Pale Nyatwali kuna ng’ombe 42,000, kaya 1,300, kwa square meter shilingi 400 ataenda kununua ardhi wapi? Leo mtu ana ekari tano unamwambia umpe shilingi milioni mbili? Tuvaeni viatu vya hawa wananchi! Tuvaeni viatu vya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mabula Dada yangu nakuheshimu, kama kuna watumishi wanakuongopea, usiingie kwenye historia ya kwenda kuwadhulumu. Kuna wamama pale wanalima, wana imani na Rais mwanamke mwenzao, msiende kumuingiza kwenye migogoro. Haiwezekani ng’ombe 42,000, wafugaji 1,000 zaidi ya 300, wataenda kununua hekari ngapi? Mtawaweka wapi? Kwa nini mnaamua kuwahamisha watu kabla hamjajipanga? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumbe macho, mtumie Jeshi la Polisi, mtishe watu kwenda kuwadhulumu watu, kwenda kuwatisha, muwaondoe huku wakiwa wana kinyongo? Taifa letu haliwezi likabarikiwa. Taifa letu haliwezi kuingia katika historia ya kuwadhulumu wananchi maskini. Kuwadhulumu wafugaji, kuwadhulumu wamama wa Nyatwali. Mimi binti yao siko tayari. Mimi binti yao niliyetoka familia maskini ya Manyamanyama, niliyelelewa na wafugaji wale sitokubali! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Nyatwali wanasema walikubali kuhama, walikuwa wana imani na Serikali yao, leo mnataka kuwalipa shilingi 400 kwa square meter siyo sawa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Taarifa

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Patrobass Katambi, Mheshimiwa Naibu Waziri.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna changamoto za migogoro ya ardhi na ndiyo maana kukaamriwa kuundwa timu ya Mawaziri wale wa Wizara Nane kwenda kushughulikia changamoto hizi, katika procedure za Sheria ya Ardhi zinavyoelekeza, lazima mfanye vikao vya consultation na wananchi husika. Vikao hivyo vilifanyika, Mawaziri hawa nane walikaa na wananchi na waliwasikiliza na katika utwaaji wa ardhi hao wanajua, tusipotoshe. Sheria ya Ardhi inaelekeza procedure za acquisition of land, kwenye Ibara ya 24 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema mwananchi unapotaka kuchukua ardhi kwa matumizi ya Serikali lazima ulipe fair and adequate compensation. Hizo procedure zinafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo taarifa ya mwisho katika utaratibu ule ule hakuna mwananchi ambaye alionewa na bado katika uthamini mwananchi anayo haki ya kukubali malipo au kukataa malipo kabla ya kwenda kwa Chief Land Valuer. Kwa hiyo, utaratibu huo upo ni suala ambalo linafanyiwa kazi na ripoti italetwa na Serikali. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Ester taarifa unaipokea?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei taarifa yake, lakini Sheria ya Ardhi inasema fidia ya haki, kwa tafsiri hiyo, shilingi 400 ndiyo fidia ya haki kwa Serikali?

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo fidia ya haki kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi? Mawaziri Nane walienda pale hamkuwatisha wananchi? Hamkuwatisha wananchi? Mnawatisha Diwani, mnawatisha Wenyeviti wa Vijiji. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Nyatwali hatutahama mpaka tupate fidia inayostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Ester, muda wako umeisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nami kwa moyo safi tu kwanza nitambue kwamba sasa hivi walau wanahabari mwanga tunauona, tumepumua kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaanza kufanya kazi kwa uhuru, tunahitaji uhuru zaidi na hili Mheshimiwa Nape umelifanyia kazi, hongera sana Kaka yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine wadau wa habari wanajua kuna mchakato wa Marekebisho ya Sheria ya Habari wanaomba usiende haraka kwenye Bunge hili. Wanaomba waweze kupata nafasi ya kutoa maoni. Wameomba sana na wanajua wewe ni msikivu, hili utalisikiliza ingawa lengo lao ilikuwa sheria mpya lakini kwa sababu kuna amendment kuna mabadiliko ya sheria wanaomba wapate muda wa kutosha kama wadau kuja kutoa maoni yao kwenye Kamati ya Katiba na Sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitambue kazi nzuri inayofanywa na vyombo vya habari na ubunifu pia kwa baadhi ya TV na redio ikiongozwa pale na mdogo wangu Diamond (Wasafi) wanafanya kazi nzuri kupitia kipindi chao cha Good Morning, kipindi cha Michezo lakini Global Online kipindi cha front page wanafanya vizuri, kuna kipindi cha TV cha 360 Clouds, Jahazi na Amplifier kinachoongozwa na Millard Ayo. Tunasema hayo kwa ajili ya kuwapa fursa wengine waweze kufanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua uwekezaji wa Azam TV wa kidijitali. Pale imeanguka siyo chini ya shilingi bilioni 15 na tunatamani Television yetu ya Taifa ifikie huko. Tunahitaji Television ya Taifa ifikie hadhi ya Al Jazeera, CNN, BBC haya yote yanawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Nape unajua mimi ni Mwandishi wa Habari, nimekaa Newsroom nilianza kama Mwandishi wa Habari Mwanafunzi mpaka Mwandamizi, ninajua changamoto za wenzangu. Asilimia 90 ya Waandishi wa Habari hawalipwi. Hao asilimia 90 ni kwenye private sector, hawalipwi na wameshazoea hiyo hali na hawana mtetezi. Mheshimiwa Nape usikubali wewe kama Waandishi ambavyo wana imani na wewe na umewapongeza kwa kazi nzuri wanayoifanya, huu Muhimili usionekane tu upo upo, upewe heshima yake. Waandishi wapewe hadhi yao kwa kazi kubwa wanayoifanya kuwahabarisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo Mwandishi ategemee source kumpa chochote, siyo kwamba anapenda, Mwandishi anatakiwa alipwe na chombo chake vizuri. Akiamua kufanya investigation story kwa maslahi ya nchi awe na uwezo huo, asiwe mnyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Nape kuna Vyombo vya Habari miaka 10 hailipi Waandishi, miaka 11 hailipi Waandishi. Kuna chombo kinadaiwa shilingi bilioni 3.5 na Waandishi. Zaidi ya miaka 10 Waandishi hawajalipwa, wafanyakazi zaidi ya 195 ambayo ni Sahara Media. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Waandishi wengine wanadai vyombo vyao shilingi milioni 100, milioni 200, milioni 300 hawalipwi lakini wapo huwasikii wakinung’unika. Wapo humu wanatuandika, wapo humu wanapeleka ujumbe kwa Watanzania nchi yao inafanya nini, kwa kinyongo lakini hawawezi kukaa nyumbani wana familia lazima watoke wakafanye kazi labda huko wataonana na watu wenye nia njema. Hii kazi siyo ya kujitolea, hii ni kazi kama Wakili, hii ni kazi kama Daktari, hii ni kazi kama Mwalimu. Wanahitaji wapate malipo yao Waandishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Nape hata michango kwa wale ambao wanapata mshahara kidogo haiendi kwenye mifuko. Hivi hatma yao hawa Waandishi baada ya kazi iweje? (Makofi)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

TAARIFA

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Napenda kumpa taarifa Dada yangu mzungumzaji kwamba anayoyazungumza ni mambo ya msingi kweli na tunajua jinsi gani Waandishi wa Habari wanavyopata taabu. Kwa hiyo nimuongezee tu siyo vibaya vilevile katika mchango wake kama ataihitaji Wizara iweze kupitia mikataba yote ya Waandishi wa Habari ili waweze kupata stahiki zao. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Bulaya.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa yake na wewe unajua Waandishi wanavyopata taabu. Hata hao ambao wanafanya, yaani kuna kampuni Waandishi wameamua tu kufanya kazi bure. Hawana mikataba Mheshimiwa Nape, hawalipwi, michango yao haiendi. Mbali na ugumu wa maisha wanayopata sasa hivi, hatma yao baada ya kustaafu hawaijui. Mheshimiwa Nape nikasema hivi Serikali na yenyewe kwenye hili inachangiaje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Nape kazi ya umiliki wa vyombo vya habari haitegemei mauzo kwenye magazeti, haitegemei labda tu TV au redio kutangaza. Vyombo vya Habari survival yake ni matangazo. Leo Serikali ukichanganya Vyombo vya Habari vya private sector na hivi vya umma mnadaiwa karibia shilingi bilioni 30. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mnapewa huduma ya matangazo, hamlipi. Sasa huyu tu kwa mfano Sahara Media ambaye anadaiwa na watumishi wake zaidi shilingi bilioni tatu anasema anawadai Serikali shilingi bilioni sita. Tukija Daily News peke yake Serikali mnadaiwa shilingi bilioni 11. Hapo sijazungumzia redio na mpaka huko kwenye level za Wilaya na Mikoa. Sasa kwa nini hamuwalipi matangazo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kweli unawezaje sasa ukaanza oparesheni ya kutaka Waandishi walipwe kama Serikali hamuwalipi Vyombo vya Habari matangazo? Inabidi muonyeshe mfano. Wamewapa huduma ya matangazo, wamewarushia live lazima muwalipe ili na ninyi mpate sasa nguvu ya kwenda kufanya oparesheni ya media ambazo hazilipi Waandishi wa Habari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Nape hilo unaliweza na Waandishi wana imani na wewe, ulikuwa radhi ku-sacrifice nafasi yako kwa ajili ya kulinda heshima ya Vyombo vya Habari. Nikuombe nenda kaanze msako wa kutetea Waandishi wa Habari wawe na mikataba, Waandishi wa Habari walipwe, michango yao iende vilevile hakikisha mnawalipa Waandishi, na vyombo vya habari vya binafsi na Serikali. Hapo TBC nilikuwa sijaitaja kabisa lakini ninataka majibu kwa nini sasa hivi kwenye bajeti ya maendeleo imepungua kwa asilimia 28? Hilo nitataka majibu, tulitarajia bajeti iongezeke zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati hapa tunasifia uwekezaji wa Azam private, huku kuhakikisha TBC inakuwa na usikivu bajeti yao shilingi bilioni 13 ili waweze kukamilisha huo mradi zimetoka shilingi bilioni tatu. Kweli tutaweza ku-compete na watu ambao wanakuja sasa hivi ili hii Redio yetu ya Taifa, Television yetu ya Taifa zifanye vizuri kama hakuna uwekezaji wa kutosha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitahitaji majibu sahihi. Tunataka tujue hatma ya Waandishi wa Habari. Hii siyo kazi ya lelemama ni kazi muhimu sana. Waandishi wa Habari wakiwa vitani wengine wanakimbia, wao wapo mstari wa mbele kutoa habari. Sehemu yoyote kwenye crisis Waandishi wa Habari watakuwa mstari wa mbele lakini hawathaminiwi kutokana na kazi wanayoifanya. Nitaendelea kulisema hili na nitahitaji lifanyiwe kazi, jambo hili la Waandishi kama la kikotoo sitaacha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mwandishi wa Habari najua kazi ya kutafuta habari, najua risk wanazozipata, najua changamoto wanazozipata, I swear sitakubali Mheshimiwa Nape. Ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; na mimi kwa kweli kama mwanamke na tunaoamini uwezo wa wanawake tuna kila sababu ya kuku-support; na In Shaa Allah, unaipeperusha bendera ya Taifa vizuri, uwezo wako si wa kutilia shaka, tunakutakia kila la heri. Ushindi wako ni ushindi wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwanza kabisa, Mheshimiwa January my brother na Naibu wake, naomba tu niwambie kwenye Jimbo la Bunda Mjini umeme umefika takriban vijiji vyote, lakini bado speed ya kuunganisha ni ndogo kufikia nyumba za watu, kufikia taasisi bado ni ndogo sana. Bunda umeshakuwa mji wanahitaji maeneo yote yawake umeme. Kwa hiyo, hilo nilisema na niliweke wazi.

Mheshimiwa Spika, kwanza Watanzania wote tumeona fahari ya Bwawa la Mwalimu Nyerere, hilo tunakubaliana kabisa. Lakini tunatamani uendeshaji wake, ukamilishaji wake uendane pia na thamani ya fedha ya Watanzania iliyowekezwa pale kwa sababu ni fahari ya nchi. Kwa sababu tunaamini ukikamilika on time utaweza kusaidia changamoto ya umeme hapa nchini, hilo hatubishi.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi nina maswali yangu, natakiwa nipate majibu ya kutosha kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa mkataba ambao mmeingia na mkanadarasi unataka Mkandarasi akichelewa kukamilisha Mradi anapaswa kutozwa tozo. Sasa huu mradi umechelewa kwa sababu ulitakiwa kukamilika mwaka 2022. Hata hivyo unatakiwa ukamilike mwaka huu, ambapo zimebaki siku 13; na taarifa zilizopo hautakamilika on time, utakwenda mpaka mwakani sijui tarehe 7 Juni. Je, kulikuwa na sababu za kutosha za mkandarasi kushindwa kutozwa tozo. Kwa nini TANESCO mpaka sasa hivi hawajamtoza mkandarasi tozo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kutokukamilisha tu mwaka 2022 alitakiwa atozwe bilioni 329. Waheshimiwa wabunge, Serikali imekuwa ikichelewa tu kumlipa mkandarasi inatozwa tozo. Ukienda kwenye miradi ya barabara, ukienda kwenye miradi ya maji, kwa nini sisi tunapata kigugumizi kwa kuchukua pesa yetu? kwa nini TANESCO wanashindwa kuchukua hii tozo? Tunajua hata kama huko mbele walikosea lakini mwaka jana walishindwa kukamilisha mradi on time, mwaka huu mradi haukamiliki on time; kigugumizi gani kinakuwepo mkandarasi asitozwe tozo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na hili tunawafanya wakandarasi waone Tanzania ni kichwa cha mwendawazimu, na kwamba wanaweza wakafanya wanavyotaka. Nilikuwa namsikia Mheshimiwa Jesca hapa, kwamba, mtu amekiri amepewa shilingi bilioni tatu halafu mambo yanaendela. Ni kwa sababu ya sisi kushindwa kusimamia mikataba yetu kwenye maeneo ambayo yanatu–favor.

Mheshimiwa Spika, na hii kwa upande wa TANESCO haijaanza leo, ukienda kwenye Symbion, ukienda kwenye IPTL ukienda kwenye SONGAS tunashida gani? Leo tena tunaona fahari ya kuwa na mradi wa Bomba la Gesi hatutaki haya yajirudie na ndiyo maana tunasema. Lazima tujifunze pale tunapojikwaa; hilo moja.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa mkataba, mkandarasi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere alipaswa kujenga miradi mbalimbali kwa ajili ya kutoa huduma za kijamii ya zaidi ya bilioni 200. Sasa mpaka sasa hivi mradi ambao unaenda kumalizika hatujui hizi huduma za kijamii zimefika wapi? Na ni haki yetu na aliji-commit, wakati haya yanaendelea yeye nasikia kwa mujibu wa mkataba, kwamba tulikubaliana anaweza tu akaongeza bei ya gharama ya mradi, na tuna taarifa ya kwamba anampango wa kufungua kesi; hili Mheshimiwa Waziri lazima utuambie limekaaje?

Mheshimiwa Spika, yeye hataki kutimiza masharti ya mkataba halafu huku yeye kwenye hicho kipengele ambacho kwa kweli mimi nakisema kibovu bado nasikia anataka kwenda kufungua kesi Mahakamani adai nyongeza wakati huku ameshindwa ku-meet vigezo vya mkataba. Tunajua kuna mitambo mingine inatakiwa ije mapema, inaingia tarehe nne mwezi August halafu bado ana-guts za kutaka kwenda kufungua kesi, hizi ni pesa za Watanzania.

Mheshimiwa Spika, na tunaamini kati ya mkandarasi anayelipwa vizuri on time ni huyo wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Kaka yangu umepewa dhamana, tunaamini tusirudie kule tulikotoka, lazima tuwasimamie hawa ili waweze kututendea haki Taifa letu na waheshimu Taifa hili lina wenyewe lina Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hizi fedha zitalipwa na walipakodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuwa na Shirika la TANESCO ni fahari, tuna miradi mikubwa, Shirika hili lisipokuwa stable hawataweza ku-manage hii miradi ambayo tuna-invest. Tuna taarifa Shirika linadaiwa sana, Shirika linadai sana, speed ya kuhakikisha hili Shirika linakuwa stable iko wapi? Nitapenda kujua, kuna deni la muda mrefu la Serikali zaidi ya tirioni mbili, kuna deni la bilioni 720 la TPDC, lakini ukisoma taarifa mbalimbali Shirika hili la TANESCO lenyewe kuhimili madeni ya muda mfupi ni shida.

Mheshimiwa Spika, tunatambua jitihada za Serikali za ku-invest kwenye miradi mikubwa, miradi ya umeme inayohitaji uwekezaji wa kutosha lakini lazima tuwe na Shirika la TANESCO imara. Nini mkakati wa Serikali wa kuhakiksha Shirika la TANESCO linakuwa imara, linaweza kujiendesha likatengeneza faida? ni aibu kukaa humu Bungeni kuimba TANESCO inatakiwa iwezeshwe, TANESCO inatakiwa iwezeshwe kimuundo, iwezeshwe kimtaji, zaidi ya miaka kumi bado tunaenda ku-invest halafu Shirika ni hohehahe? Yaani ni sawa unanunua furniture kwenye nyumba ya udongo, furniture kali lakini nyumba ina ufa.

Mheshimiwa Spika, lazima hivi vitu vinaenda sambamba tuna-invest kwenye miradi tunahakikisha Shirika letu linakuwa stable.

Waheshimiwa Wabunge yasije yakatukuta kama ya Afrika ya Kusini, leo wana mgao mkali kwa sababu gani? Shirika lao limeyumba, Shirika lao haliko stable. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Spika, hii miradi tunayowekeza mikubwa ya gharama nafuu lazima Shirika letu litakaloenda kusimamia miradi hii liwe na uwezo wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, Kingine Mheshimiwa Waziri tunaomba utupe status ya umeme nchini ikoje? nilikuwa kwenye kamati Lindi, zaidi ya mara kumi umeme ulikatika. Umemskia Mbunge wa Kahama, umesikia taarifa iliyotolewa na Mbunge wa Mkoa wa Songwe, shida ipo lazima kama Taifa tuambiwe tatizo liko wapi maana kuna manung’uniko; ooo uchakavu wa mitambo, sijui nini;

Mheshimiwa Spika, sasa lazima kama Wabunge Wawakilishi wa Wananchi tupate maelezo sahihi status ya umeme nchini ikoje. Tunafurahi sasa hivi mkakati wako wa gesi lakini bado spidi ya uunganishaji wa gesi kwenye viwanda ni ndogo sana. Tunataka tujue kwenye viwanda peke yake zitatumika kiasi gani kujenga miundombinu ya gesi ili sasa viwango vyetu viwe na uhakika wa kupata umeme wa kutosha na waweze kuchangia uchumi kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa niwapongeze kwa uteuzi, dada yangu, Mheshimiwa Balozi Dkt. Pindi Chana, nimetoka naye mbali UVCCM kule, najua uwezo wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze Binamu, rafiki yangu, wasanii wanasema ile Master’s ya Uingereza walikuchangia, kwa hiyo wanataka waone matunda yake. Wanajua uko sehemu sahihi ya kubadilisha industry yao lakini na uwe mfano kama kijana wa Kitanzania ambaye umepitia huko unajua changamoto zao, matokeo wanataka wayaone; mimi sina shaka na wewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi kwanza nianze na jambo moja, Mheshimiwa Waziri wa Fedha tunaomba, hii michezo ya kubahatisha iende kwenye Wizara husika. Tunalia hapa watu hawana bajeti, wewe una vyanzo vingi vya fedha; una majengo, una mambo ya matrilioni huko, mabilioni, sasa hawa ambao vyanzo vyao vidogo hata michezo ya kubahatisha? Kwa sababu hata hicho kinachokwenda kinakwenda kama hisani, wapewe fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na Waheshimiwa Wabunge, tupambane humu ndani hii Wizara iheshimike kama tulivyoipambania Wizara ya Maendeleo ya Jamii. Hii Wizara itatengeneza ajira mpya, hii Wizara ikipewa fedha za kutosha Taifa litakuwa na furaha. Watanzania wanapenda michezo, tutapata Timu bora ya Taifa; haviwezi kuja hivihivi kama tusipowekeza. Lazima Wizara hii ipewe fedha ya kutosha iwe na vyanzo vya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amesema Mheshimiwa Tarimba hapa, wanakusanya mabilioni kwenye michezo ya kubahatisha halafu wanapewa vipesa vidogo, haiwezekani. Hicho ni chanzo chao cha sahihi, wapewe waweze kuwekeza maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waheshimiwa hapa wanasema tunawaona tu wasanii wakubwa, ni kweli, huko mikoani kuna wasanii wengi. Kama Wizara haina fedha itawezaje kutengeneza mazingira mazuri ya kuwasaidia wale wasanii wengine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Mara tuna wasanii bwana; kuna Lady Jay Dee pale Bunda, lakini alifika hapo kwa taabu, hatuhitaji wengine wa-suffer kama Lady Jay Dee. Tuna Isha Mashauzi, Mkurya wa kwanza kuimba taarabu. Tunahitaji Wakurya wengine kule tuwaibue waimbe taarabu. Tuna Getrude Mwita, ‘Kibibi’, anaigiza vizuri. Tunahitaji hii Wizara iwezeshwe ili watokee akina Kibibi wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bila kuwekeza, siyo kwenye football peke yake, kwenye sanaa, kwenye utamaduni, hii Wizara ikiwekeza vizuri tunaamini tutapata wasanii wengi walio mikoani huko watatambulika na hii nchi itajivunia wasanii mbalimbali kutoka pande mbalimbali za nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mara sasa hivi Mungu ametujalia tuna timu mbili kwenye Ligi Kuu; tuna Biashara United. Lakini Uwanja wa Musoma ni mbovu, unahitaji ukarabati, una jukwaa moja tu, zikichezwa pale timu kubwa mapato yanakuwa madogo, kwa hiyo klabu inakosa mapato ya kutosha, tunahitaji uwanja ukarabatiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunda tuna Uwanja wa Sabasaba, tuna Bunda Queens, wameshinda kucheza Ligi Kuu ya Wanawake, lakini Uwanja wa Sabasaba hohehahe; ni lini mtaukarabati Uwanja wa Sabasaba ili Timu ya Bunda Queens iwe na uwezo wa kucheza uwanja wa nyumbani? Hayo mambo tunahitaji majibu sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabondia wetu wanahitaji na wenyewe wawe na viwanja vyao. Zamani ukisikia bondia anapigana unasikia DDC, viwanja vyao. Watengenezewe mazingira mazuri, na tunapata mapromota hapa akiwemo Mheshimiwa Mwakagenda, mabondia wamechoka kwenda kupigania kwenye viwanja vya mpira; hilo ni jambo sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna jambo la msingi, sasa hivi wakipata matamasha kwenda kupigana nje ya nchi anatakiwa kwenda peke yake; anawezaje kushinda bila kocha? Iwe kama timu za mpira wa miguu, inaposafiri timu inakuwa na kocha na benchi la ufundi. Ukienda wasanii akisafiri anakuwa na meneja wake na dancers wake. Kwa nini kwa upande wa mabondia anatoka yeye, yaani atoke Mwakinyo peke yake bila benchi lake la ufundi, bila kocha wake; hii haiwezekani. Mchezo wa ngumi umekua hivyo lazima upewe thamani yake; hilo ni jambo la msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka tujue mchaka wa Vazi letu la Taifa umeishia wapi? Iliundwa kamati, imeyeyukia wapi? Yaani Watanzania wakiwa wanadai Vazi la Taifa ndiyo mnaanza kuwakusanya wanamitindo mbalimbali. Mchakato wa Vazi la Taifa umeishia wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani sasa hivi kila mtu anaamua tu anachagua vazi analolipenda, mimi na mwili wangu najua nikivaa Kihindi hapa nikipiga Sari, Punjabi ntakaa sawa, mwingine anachagua tu Vazi la Uganda, Vazi la Rwanda. Jamani, Taifa hili lina historia yake, tuna mavazi mengi, tupendekeze tukija humu Bungeni hata siku moja moja na sisi kama Wabunge tuna Vazi letu la Taifa. Lazima muweke historia ya kumaliza mchakato wa Vazi la Taifa; hilo ni jambo la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine, Mheshimiwa Mwana FA na Mheshimiwa Waziri, wewe ume-perform nchi mbalimbali, tunahitaji arenas. Leo hii msanii mkubwa ndiye mwenye uwezo wa kwenda kukodi pale Mlimani City. Ukumbi ule si chini ya milioni 30, bajeti yake ili aweze kuandaa tamasha anatakiwa atenge kama milioni 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na arenas nyingi hata ya watu 20,000, tukiwa na arenas za kutosha ushindani utakuwa mkubwa, hata bei itapungua. Watakaoukuwa na uwezo wa ku-meet standard ya kwenda kwenye arena watakuwa wengi, gharama itapungua…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, niseme wazi mimi ni Mwandishi wa Habari na nitawasemea wanahabari, changamoto zao nazijua na nimeziishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na kwa kurudi kwako kaka yangu kuna nafuu, watu wamepata hope waandishi wenzangu. Na kwa kauli ya Mheshimiwa Rais imetoa hope kwa ile kuonesha dhamira. Tunahitaji dhamira Mheshimiwa Waziri yako na Mheshimiwa dhamira ya Rais sasa ije kwenye vitendo kwa kuleta mabadiliko ya Sheria ya Huduma ya Habari ya mwaka 2016. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wewe unajua mbali ya kwamba kuna unafuu lakini bado kwenye maeneo mengine waandishi wanatishwa. Bado waandishi hawafanyi kazi kwa uhuru. Mheshimiwa Waziri unajua, leo hakuna investigation story si kwenye print media wala kwenye electronic media. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hizi Makala ambazo zinaandikwa ni za kawaida. Sheria hii ililetwa kutakuwa na mijadala ya kujenga, ya kukosoa Taifa letu lakini ya kujenga. Tunataka turudi enzi hizo, tunataka tuone Makala za uchunguzi, tunataka tuone vipindi mbalimbali kwenye Redio na Televisheni ambavyo wachambuzi watakuwa huru kwa maslahi ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hayo yote Mheshimiwa Waziri hayawezi kutokea kama hakutakuwa na Sheria bora ya kuwafanya waandishi wa habari kwenye print media kwenye electronic media wanafanya kazi kwa uhuru. Na kufanya kazi kwa uhuru kukiwa na uwazi ndiyo Taifa letu linasonga. Lakini kwa dhamira tu, leo anaweza akamaliza Mama Samia muda wake ana dhamira njema, wewe una dhamira yako ukatoka lakini akaja wengine ambao hawana dhamira njema bado tukarudi kule kule kwa waandishi kuteswa, kwa waandishi kupigwa, kwa waandishi kunyanyaswa, kwa waandishi kunyimwa habari kwa maslahi ya watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niombe Mheshimiwa Waziri, najua umeanza kukutana na wadau wa habari ni jambo jema. Lakini nilikuwa naomba zile Sheria zenye ukakasi Serikali ndiyo mzichukue, mzibadilishe kwa sababu ndiyo zinawanyima fursa waandishi wa habari. Kwa mfano Mheshimiwa Waziri wewe unajua, natolea tuu mfano kwenye Sheria ya Huduma ya Habari Kifungu cha 19(20)(21) ambacho chenyewe kinazungumzia kinawatambua watu gani ni waandishi wa habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye tasnia yetu pia tunawahitaji Wanasheria, kuna watu wataandika habari zinazohusu Sheria. Tunawahitaji Madaktari ambao wataandika habari za afya. Tunawahitaji Wachumi ambao watafanya analysis ya masuala ya kiuchumi. Lakini kwa sheria hii inataka mtu mwenye degree ya Sheria ya udaktari akija aanze tena degree ya habari, hapana. Sisi kwetu tuna taratibu zetu, kwa mfano mimi wakati nipo uhuru pale tulikuwa tunasoma media law and ethics kwa sababu gani? Tunajua lazima waandishi wa habari wapate training mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hawa wakiwepo Wanasheria wamekuja kutaka kufanya kazi ya habari watapewa mafunzo ya miiko, maadili namna gani ya kuandika habari lakini bado wana taaluma zao. Sasa hayo Mheshimiwa Waziri ni mambo ya muhimu sana na leo kwa mfano kuna kina Jenerali Ulimwengu ni Mwanasheria lakini ni Mwandishi nguli. Tuna Kibanda ni Mwalimu by profession lakini ni waandishi wazuri. Kwa hiyo, na sisi tunawahitaji watu wa namna hiyo kuja kufanya uchambuzi wa kina kwenye tasnia yetu. Lakini watapewa miongozo inayohusu habari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano pia, Mheshimiwa Waziri wewe unajua kuna Kifungu cha 5(e)(8)(9) kinazungumzia masuala ya leseni. Hiki kifungu kinatoa mwanya kwa Mawaziri wenye nia mbaya kufungia vyombo vya habari. Hiki kifungu ni kifungu kibaya kuliko vifungu vyote, tunaomba vifanyiwe kazi. Gazeti linatakiwa lisajiliwe tu, sasa kila mwaka leseni, kila mwaka leseni mtu ana kampuni hiki kifungu kibaya kinatengeneza mazingira ya kufungia vyombo vya habari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mzigo mzito kapewa Mnyamwezi wakati hii Sheria mbovu inatungwa ulikuwepo wewe na umeiona na imetestiwa imekuwa mbaya. Mzigo huu unao wewe mwenyewe wahakikishie kipindi kile kilikuwa kingine, hiki kingine, rekebisha hii Sheria sisi waandishi wa habari tunataka tuwe huru, tulikosoe Taifa letu kwa maslahi ya kujenga ili nchi yetu iende kama nchi zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na mimi niwapongeze watoto wetu Serengeti Girls kwa kutufanya tutembee kifua mbele, tunakwenda kushiriki michuano ya dunia. Lakini pia nimpongeze Waziri na Naibu wake mmeanza vizuri tuna matarajio na ninyi, tupeni raha watanzania wanapenda michezo wanapenda wasanii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muda mrefu sana tumekuwa tukitamani kwenye mpira wa miguu kusomeka kwenye ramani ya dunia, timu ya Serengeti Girls wametuonesha, kama Taifa Serikali inapaswa kuandaa bajeti stahiki ya kwenda kuwawezesha timu yetu kufanya vizuri, isiwe sasa utashi wa Rais peke yake, iwe commitment ya Serikali kwa ujumla. Hawa watoto wamejiwezesha sasa twende tuka-invest tuchukue Kombe la Dunia lije nyumbani. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitamani kwa wanaume wamefanya yao kwa kiwango chao, hawa mabinti tuwekeze, tumeona commitment ya timu za wanawake, dada zao kwa Afrika tuliona walivyofanya vizuri COSAFA kama sikosei wamefanya vizuri, hawa na wenyewe wanafanya vizuri. Hii inatukumbusha twende tuka-invest soka la wanawake kuanzia level za wilaya, kuanzia mashuleni na Mheshimiwa Waziri tumerudisha michezo mashuleni kuna timu za wanawake za mpira wa miguu? Mpaka tulalamike wanawake ndio tuanze kusaidiwa, tuanze kupewa fursa kwenye maeneo mbalimbali. Sasa hawa wameonesha uwezo, wakati tunarudisha michezo mashuleni tusiangalie mpira wa miguu kwa wanaume peke yake, tuanze ku-invest kwenye mpira wa miguu kwa wanawake kwenye level za mashule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tumeona commitment ya mtoto wa kike, sisemi kama wanaume hawafanyi vizuri, lakini hawa wamepewa nafasi na wameonesha. Leo tunatamba tutawaona timu yetu ya Serengeti Girls kwenye ulingo wa kidunia, sio jambo dogo, tumetamani hiyo nafasi. Sasa isiwe utashi wa Rais iwe commitment ya nchi. (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo wanafanya nchi zingine.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Bulaya kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nami nampa taarifa Mheshimiwa Bulaya kwamba ni kweli anavyochangia kwamba Serikali lazima itenge bajeti sio utashi wa Rais. Mathalani tumeona wenzetu wenye ulemavu Tembo Warriors wanakwenda kushiriki World Cup, lakini wana bajeti constrained. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma tuliona Rais aliwaita Ikulu wakati wameshiriki katika ile level ya Afrika, sasa wanakwenda World Cup lakini wana bajeti constrained, kwamba wangewatengea specifically kwa kuwa kuna bajeti kwa sababu ya kusaidia makundi haya inakuwa inasaidia sana. Kwa hiyo, nilikuwa nataka kumpa hiyo taarifa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Matiko nilikuwa nasikia mipasho, mipasho ulikuwa unamaanisha nini? Mipasho ya nani? Umesema mipasho ya Rais sijakuelewa maana yako ni nini?

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, utashi wa Rais, lakini tuwe na bajeti kabisa imetengwa kwa haya makundi ambayo unakuta wamefikia level ya kwenda kwenye World Cup na kadhalika. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Bulaya unaipokea taarifa?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naipokea maana leo wanaweza wakawa na Rais ambaye ameona kuna jambo jema kwenye timu zetu, kesho akaja Rais mwingine ambaye sio kipaumbele, lakini tukiwa tuna mpango mkakati kama nchi itatusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie netball (mpira wa pete); hivi kama Serikali mpira wa pete tunauchukuliaje? Na ninashukuru leo viongozi wa CHANETA wako hapa, wamechaguliwa na niwapongeze, wameanza kujitambulisha. Lakini bado hatujawa na mkakati wa kufufua netball kwenye nchi yetu, tuwawezeshe CHANETA, ni chama kidogo hiki hatuwezi kulinganisha na TFF. Hawana wadhamini, hawana fedha, watawezaje kwenda kuangalia vipaji mikoani na wilayani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaona je, na kwa sababu unahusu wanawake; tuanze kuuliza ni kwa sababu na wenyewe unahusu wanawake?

Mheshimiwa Waziri tuna wachezaji wazuri sana wa netball wako maeneo mbalimbali, hawapati fursa unakuta mpaka Wabunge waandae mashindano. Kuna muda mwingine mashindano yanakwama hawana fedha, tuiwezeshe CHANETA, tuanze sasa kuhamasisha na kuandaa mashindano mbalimbali level za wilaya ya netball. Tukarabati viwanja vya netball na kwenye mashindano yaliyopita hivi hivi kimkandamkanda tumepata wachezaji watatu kwenye timu ya Afrika. Je, tukiandaa, je, tukijipanga tutafika wapi? Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri nadhani mmenisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona kwenye hotuba yako umezungumzia kiwanja cha mpira wa miguu hapa Dodoma. Nilikuwa nataka kujua hiki kiwanja kinahusiana na ule Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambao zile fedha za huduma kwa jamii? Ndio nilitaka nijue na kama sio hiyo kwa nini? Kwa sababu na wenyewe upo na miongoni mwa fedha zilizotengwa ni shilingi bilioni 262 ukiwepo na ujenzi wa uwanja wa mpira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama sio hizo je, huyu mkandarasi kagoma kutoa hizi fedha na kama Serikali tunasemaje? Nataka kujua hilo yaani kama sio na wakati wameshaingia makubaliano na mradi unakamilika Juni 13 na hawajajenga uwanja, tunataka kujua je, huo uwanja utajengwa lini na makubaliano yanasema hivyo kuwa wajenge kiwanja cha michezo. Tumeamua kumuacha tu atuchezee tu kama nchi na tumeingia makubaliano, hilo pia nataka kujua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haraka haraka Baraza la Sanaa liko dhooful-hali, halina fedha. Ukiangalia mali tu za muda mfupi walizonazo milioni 116, madeni waliyonayo tofauti na mali milioni 350, mtaji wa kujiendesha milioni 234. Hawa ndio wanashughulikia tasnia nzima hii ya Sanaa, hawana Bodi hawa. Je, tumeweka hii sanaa yetu rehani na tunaona vipaji mbalimbali vya vijana wetu. Chombo chao kipo dhooful-hali kiasi hiki? Haya mlipanga kuwapa shilingi bilioni 1.1 mkawapa shilingi milioni 700 tu wajiendesheje? Sanaa imekua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama chombo chao tu hatukipi pesa, tuanze kulia kwenye timu za wanawake, tuanze kulia kwenye netball, tuanze kulia kwenye football, mpaka kwa wasanii ambao na wenyewe wanaliwakilisha vema Taifa letu? Hili suala la Bodi liko kwenye mikono yako, hawana Bodi huu mwezi wa nne, wako dhofuli hali, pesa hawana na ipo kwenye ripoti ya CAG ya mwaka huu, wapeni pesa Baraza la Sanaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)