Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Oran Manase Njeza (3 total)

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Wakati tunaelekea kwenye msimu mwingine wa kilimo na mvua zimeshaanza kunyesha kwenye maeneo mengi ya nchi yetu likiwemo Jimbo langu la Mbeya Vijijini, lakini pembejeo za ruzuku za kilimo bado hazijawafikia walengwa. Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kuwa hizo pembejeo za ruzuku zinawafikia wakulima kwa muda muafaka?
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:- (Makofi/ kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya kilimo imeweka utarabu wa kusambaza pembejeo kwenye maeneo yetu kote nchini, pembejeo za mbegu na mbolea.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeamua msimu huu wa kilimo, kuanzia mwaka huu, kutumia taasisi inaitwa Tanzania Fertilizer Cooperation Company ili kupeleka mbolea, lakini pia mashirika mengine kusambaza pembejeo za aina nyingine. Mashirika haya tayari yameshakaa na Wizara ya Kilimo kwa pamoja ili kuweza kuratibu vizuri usambazaji wa pembejeo mpaka kwenye ngazi za vijiji na kuweza kuwafikia wakulima kabla ya msimu wa kilimo kuanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika mwezi uliopita tumeshatoa fedha kwa ajili ya kununua pembejeo na tumekabidhi taasisi zote ambazo nimezitaja ambazo pia zenyewe zinaweza kupata Mawakala kwenye ngazi ya Wilaya kule ili kuwafikishia wananchi kwenye ngazi ya vijiji na msimu huu wa kilimo utakapoanza, wakulima waweze kupata hizo pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Watanzania wote ambao kweli tumejikita kwenye kilimo kwamba, Serikali itaendelea kujitahidi kuhakikisha kwamba pembejeo zinawafikia wakulima kwa wakati na hasa wakati huu ambao mvua zimeshaanza kunyesha katika baadhi ya maeneo, kabla ya mazao husika kulimwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kusimamia na tutaendelea kutoa fedha zaidi ili tuweze kupeleka mbolea, mbegu za mazao ambayo yako kwenye orodha ya pembejeo kama ambavyo tumekusudia.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata fursa ya kuuliza swali kwa Waziri Mkuu.Mheshimiwa Waziri Mkuu, pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Kamati ya Mawaziri Nane ya kutatua migogoro kati ya hifadhi, hususan TFC na TANAPA, lakini kuna vijiji ambavyo bado havijafikiwa vikiwemo vijiji katika Wilaya yaMbeya. Je, ni lini Kamati hii itarejea kukamilisha hilo zoezi muhimu kwa maeneo yaliyobaki nchi nzima? Nashukuru sana.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, Serikali iliunda timu ya Mawaziri Nane kwa ajili ya kuhakiki vijiji ambavyo vina changamoto au migogoro kati ya vijiji hivyo na hifadhi. Mnatambua Waheshimiwa Wabunge tulipata taarifa za awali za utekelezaji huo na bado kazi hiyo inaendelea.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Njeza anahitaji kujua lini kazi hiyo itakamilika, ili tuweze kwenda kule Mbeya. Nataka nimhakikishie kwamba, kazi iliyofanywa awali ambayo ilibaini vijiji vipatavyo mia tisa kama 75 hivi na kati ya hivyo ilithibitika kuwa vijiji mia tisa na 20 havikuwa na matatizo na bado vilikuwa vinatakiwa kuishi huko kwenye maeneo ambayo tuliyahifadhi, lakini hayana tija. Bado Serikali inakusudia kutambua vijiji kadhaa vyenye migogoro ya aina hii kati ya vijiji na hifadhi, pale ambapo tunaona kwamba, uhifadhi wake hauna tija kwa malengo yaliyokusudiwa, vijiji hivyo vitapata nafasi ya kuendelea kushiriki shughuli za kijamii kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, pindi Kamati itakapokamilisha, tutakuja kutoa taarifa nyingine tena baada ya taarifa ya awali. Sasa, naielekeza Kamati ile pia, kuweka mpango kazi wa kwenda Mbeya Vijijini kuona huko ambako Mheshimiwa Mbunge anasema bado hatujafika, waone vijiji hivyo, lakini pia, aina ya mgogoro uliopo na nini tufanye baada ya kuhakiki. Kwa hiyo, Kamati ya Mawaziri wale nane itakapokamilisha kazi hiyo tutaipata.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito, tunatambua tuna migogoro mingi, iko migogoro ya mipaka kati ya vijiji na vijiji vyenyewe, iko migogoro ya wafugaji na wakulima, bado nielekeze kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, hususan Waheshimiwa Wakuu wa MIkoa, Wakuu wa Wilaya, lakini tunashuka chini kule kwa Watendaji wa Kata na Vijiji kuhakiki migogoro hii na tujiridhishe kuwa inakamilishwa hukohuko kwenye ngazi hiyo, badala ya kutegemea Mawaziri ambao wako hapa Dodoma wasafiri waje kwenye vitongoji na vijiji badala ya kuwa wamekamilisha kule na Mawaziri wapate unafuu wa kutekeleza hili. Ikifika hatua hiyo ya kila mmoja kuwajibika kwenye nafasi yake hii migogoro itapungua kwa kiasi kikubwa, kama sio kuimaliza kabisa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa kuna miradi mingi ya miundombinu inayosubiri kutekelezwa kwa bajeti ya Serikali na bajeti ya Serikali; na bajeti ya Serikali imekuwa inatengwa kwa kutumia fedha za ndani na fedha za nje, lakini mfumo huu umeonesha kuchelewesha miradi na hata kupelekea gharama ya miradi kuwa kubwa:-

Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kuanza kutumia mfumo wa PPP au mfumo wa EPC plus finance ambao ni mfumo wa Engineering, Procurement na Construction ambao umeonesha mafanikio makubwa sana kwa nchi za Afrika Mashariki na hata SADC ili kupunguza gharama za utekelezaji? Ahsante sana.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara zake, tunaleta bajeti zetu hapa na Waheshimiwa Wabunge mnapitisha bajeti hizi. Siwezi kusema kwamba bajeti hizo hazitoshi, lakini najua mahitaji ni makubwa, ni kweli tunahitaji fedha nyingi; na baadhi ya miradi tunapoitekeleza mwishoni mwa mwaka, mingine tunakuwa hatuikamilishi kwa sababu ya mwenendo wa makusanyo ambayo tulikuwa tunategemea kukusanya, kiwango hicho cha fedha ambacho tulikiomba hapa Bungeni, kinaweza pia kisitoshe.

Mheshimiwa Spika, iko mifumo mingine ambayo inawezesha pia kukamilisha bajeti zetu tunapopata fedha kutoka nje ya bajeti inayotegemea mapato ya ndani, kwa sababu bajeti zetu zinategemea mapato ya ndani, na pia tuna marafiki zetu wanaongeza mtaji na tunatekeleza majukumu yetu. Hii ndiyo tunafanya kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, sasa tunapokwenda kukusanya na tusifikie malengo, tunatafuta njia nyingine ikiwemo na hiyo ya PPP ambayo kwa muda mrefu tumeitekeleza, lakini imekuwa ngumu kidogo kutekeleza na tumebadilisha na sheria. Leo Mheshimiwa Njeza amependekeza mfumo wa EPC plus finance, najua Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi ameizungumzia sana mfumo huo juzi hapa wakati wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, mfumo huu unatafuta mwekezaji ambaye atakuwa tayari kutekeleza mradi wa aina fulani, anautengenezea mchoro wake, tunakaa naye, tunakubaliana naye, tunampa kazi hiyo ya manunuzi, ujenzi; na tunapokwenda kujenga, gharama ya mradi anaitumia yeye, na sisi tunaupokea mradi kwa yeye kuujenga, halafu kuufanyia kazi na wakati mwingine anaweza kuurudisha kwetu tuutumie baada ya kuwa ametumia kwa kipindi fulani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, miundombinu ile inabaki kwetu sisi. BOT (Build, Operate and Transfer System), hiyo inaweza kuwa inaendelea kutumika kwa utaratibu huo. Kwa hiyo, mfumo huo tunaukubali Mheshimiwa Njeza, ushauri wako nakuahidi tunauchukua, ni mfumo mzuri na Waziri wa Ujenzi yupo, Wizara ipo, itatumia mfumo huo na Wizara ya Fedha ipo, itaangalia mwenendo wa mapato yetu, nao ndio wanaoweza kuangalia mfumo huo tunaweza kupata kwa kiasi gani; na kama tunakopeshwa gharama yake ni kiasi gani? Kwa maana hiyo, tutakubali mfumo huo pale ambako tunaweza kupata mkopo huo wenye gharama nafuu ili tuweze kutekeleza miradi yetu.

Mheshimiwa Spika, nataka nimwakikishie Mbunge na Waheshimiwa Wabunge kwamba ile miradi yetu tuliyoipendekeza kuitekeleza kwenye bajeti hii, hata kama hatutakusanya kwa kiwango cha kutosha, mapato ambayo tunayo, tutatumia mfumo ambao Mheshimiwa Njeza ametupendekezea hapa kwa sasa, ahsante. (Makofi)