Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Frank George Mwakajoka (47 total)

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kujua barabara ya Tunduma - Mpemba yenye kilometa 12 itajengwa lini na Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi kwa sababu barabara ile inasababisha msongamano mkubwa sana wa magari kwenye Mji wa Tunduma na wananchi kushindwa kutimiza majukumu yao. Kwa hiyo, nataka Waziri atueleze ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwenye Mji wetu wa Tunduma haraka iwezekanavyo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii inahitaji takwimu, ninamwomba Mheshimiwa Mbunge, avute subira tuwasiliane na wataalam ili tuweze kumpa jibu lililo na uhakika.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa sababu matatizo ya maji katika jimbo langu yanafanana sana na Jimbo la Kigoma Kaskazini, ninapenda nimuulize Mheshimiwa Waziri swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali hii itakamilisha Mradi wa maji katika Mji wa Tunduma kwa sababu imekuwa inaahidi mara nyingi kwamba itatengeneza maji na hata wakati Mheshimiwa Rais anaomba kura kwa wananchi pia alisema kwamba ataweza kuwaletea maji haraka iwezekanavyo ndani ya mwaka mmoja mradi utaanza kutekelezwa. Leo hii kuna kampuni ambayo tayari imekubali kujenga…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwakajoka, swali si umeshauliza? Nadhani swali umeshauliza, kwamba huo mradi utakamilika lini?
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka nikumbushe kidogo kwa sababu kuna kampuni leo imekuja hapa na mradi ule umeshapitishwa na Wizara lakini tunashangaa Wizara ya Fedha hawataki kukubali mradi ule uanze kujengwa haraka. Kwa sababu mradi ule ulitakiwa uanze kujengwa mwanzoni mwa mwaka huu lakini mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea. Tunataka kupata majibu.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuwapatia wananchi wote maji safi na salama kwa kiwango cha asilimia 85 ifikapo mwaka 2020. Kwa hiyo, naomba nikuhakikishie, hayo unayoyazungumza ni historia, Serikali inakwenda kutekeleza Mradi wa Maji Tunduma ambao nina uhakika na tuwashauri wananchi wa Tunduma waiamini Serikali ya Awamu ya Tano. Ahsante.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Barabara hii ahadi yake ilikuwa ni kujengwa kwenye bajeti ya mwaka 2009/2010 na daraja lile ilikuwa ni 2009/2010, lakini mpaka leo daraja lile halijajengwa. Je, majibu ya msingi ya Mheshimiwa Waziri yataleta matumaini kwa wananchi wa Jimbo la Momba hasa eneo la bondeni kwamba itaanza kujengwa mapema mwaka 2016/2017?
Swali la pili, Momba ni Wilaya mpya ambayo inaunganisha Mji wa Tunduma na kutoka Tunduma kuelekea Makao Makuu ya Momba, eneo la Chitete ni Kilometa 120. Je, Serikali inasema nini kuhusiana na kutujengea daraja katika Mto Ikana katika Kijiji cha Chitete, Kata ya Msangano ili wananchi wa Tunduma waweze kufika kule wakiwa wanatumia barabara ile ambayo itakuwa na kilomita 68?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema na kama nilivyoelekezwa na Waziri wangu wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ahadi yake kwa Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, Mbunge wa Kwela, ambaye ndiye amekuwa akifuatilia ujenzi wa daraja hili pamoja na barabara kwa upande ule wa Mkoa wa Rukwa, utatekelezwa kama ulivyoahidiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali dogo la pili linalohusu Mto Ikana, namwomba Mheshimiwa Mbunge alilete swali hili rasmi Wizarani ili Watalaam walipitie kabla mimi Naibu Waziri sijatoa commitment ili commitment yangu izingatie ushauri wa Watalaam.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami napenda kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Tunduma ni lango kuu la nchi za Kusini na Kati mwa Afrika na kwa sababu Mheshimiwa Waziri amenihakikishia kwamba mradi mkubwa wa maji utajengwa kwenye Mji wa Tunduma lakini kuna mradi ambao ulijengwa mwaka 1973, mradi wa maji wa kutega kwenye Kijiji cha Ukwire ambapo ulikuwa unahudumia Kata za Mpemba, Katete na Chapwa na sasa hivi mradi ule hautoi maji ya kutosha. Ni lini Serikali itakwenda kukamilisha mradi ule wa Mpemba ambao unalisha kata tatu katika Mji wa Tunduma?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Mji wa Tunduma tayari study imeshafanyika kwa ajili ya kuweka mradi mkubwa wa maji. Tuna mfadhili ambaye ameshajitokeza, tunaongea naye, Serikali bado inafanya mazungumzo na yeye kwa sababu alikuwa amekuja na masharti ambayo yanaweza yasiwe na manufaa kwa upande wa wananchi wa Tunduma.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba moja, tunaweza tukapitia mradi huo mkubwa unaokuja, lakini pili ni kwamba mpango wa Serikali ya Awamu ya Tano inahakikisha kwamba inakarabati miradi yote iliyokuwa imejengwa hapo awali ili kuondoa upungufu ukiwemo mabomba ya maji ambayo yamechakaa, mitambo ambayo imechakaa na vilevile kuongeza huduma kwa sababu kila kunapokucha watu wanaongezeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika programu hiyo tutahakikisha kwamba, hayo maeneo Mheshimiwa Mbunge ambayo anayataja nayo tumeyapitia ili kurudisha upatikanaji wa maji ambao umepungua kwa sasa na hasa kwa kuzingatia kwamba Mji wa Tunduma unapanuka sana. Nafikiri upunguaji huo wa upatikanaji wa maji ni kutokana na kwamba watu wameongezeka katika Mji wa Tunduma.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wetu wanavyokwenda katika nchi ya Zambia hasa katika Jimbo la Copperbelt wamekuwa wanakamatwa wakiwa stand na wanapelekwa gerezani bila kupelekwa Mahakamani. Je, Serikali inasema nini kuhusiana na jambo hili kwa sababu kuna vijana wengi sana ambao wako magereza na hawajapelekwa Mahakamani mpaka sasa hivi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili nalipokea na Wizara yangu pamoja na Wizara ya Mambo ya Ndani tutalifanyia kazi, ahsante.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii ili niweze kuuliza swali la nyongeza kwa niaba ya wananchi wangu wa Mji wa Tunduma. Swali la kwanza; Mji wa Tunduma ni mji uliopo mpakani mwa Tanzania na Zambia na ni lango kuu la nchi za Kusini na Kati mwa Afrika. Kwa tafsiri hiyo ni kwamba wageni wote kabla hawajingia katika nchi ya Tanzania ni lazima wapitie Tunduma kutoka katika nchi hizo.
Je, Serikali ina mpango gani wa makusudi na wa haraka wa kupima ardhi katika Mji wa Tunduma ili kuondoa ujenzi holela unaoendelea kwa hivi sasa? (Makofi)
Swali la pili; nini mwongozo wa Wizara ya Ardhi ikishirikiana na TAMISEMI kupitia Halmashauri zetu kwenye Idara ya Ardhi ili kutoa fursa kwa Halmashauri kukopa fedha katika taasisi za fedha, lakini pia kukubali makampuni binafsi ambayo yanaweza yakapima ardhi mfano UTT katika maeneo yetu ili kuhakikisha kwamba tunapunguza ujenzi holela katika maeneo yetu ya Mji wa Tunduma na maeneo yote nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza, nikubaliane naye kwamba ni kweli Tunduma ni lango kuu na lipo mpakani na uingiaji wa watu pale ni mkubwa sana kwa hiyo panahitaji kuwa na mipango iliyo thabiti. Ameuliza tuna mpango gani wa kupima ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, jukumu la kupima ardhi siyo la Wizara peke yake, Halmashauri zenyewe zinatakiwa kuwa na mipango yake ambayo inakuwa imeandaliwa. Wizara inakwenda kutoa msaada hasa wa wapimaji labda na vifaa kupitia Kanda pale ambapo Halmashauri imeshindwa yenyewe kutekeleza jukumu hilo. Kama mna mpango huo tayari Tunduma, Wizara yangu itakuwa tayari kushirikiana nanyi kuhakikisha kwamba maeneo yale yanapimwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ametaka kujua nini mwongozo wa Wizara katika suala zima la upimaji kwa kutumia mashirika au makampuni binafsi ukatolea mfano wa UTT. Naomba niseme tu kwamba, Wizara tayari imeshabainisha makampuni 55 na orodha kamili tunayo na Wabunge kama mtahitaji tutawatolea copy tuwape ili muweze kushirikiana nayo kwa sababu baadhi ya makampuni mengine siyo wakweli katika kufanya kazi, lakini tunayo ambayo tumeainisha yapo makampuni 55 ambayo tumeruhusu yanaweza kufanya kazi na Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa ni ninyi wenyewe Waheshimiwa kuzungumza na yale makampuni na kuweza kukubaliana namna bora ya kuweza kufanya upimaji. Kwa sababu wakati mwingine yale makampuni yanaweza yakapima kwa kutumia rasilimali zao, lakini kuna namna ambavyo Halmashauri inakubaliana nao wawalipe kiasi gani katika kazi wanayofanya au wanaweza wakawasiliana na wananchi moja kwa moja wenye mashamba makubwa, lakini kupitia Halmashauri kujua mpango wenu ukoje katika maeneo yale, wanakubaliana namna ya kulipana katika zoezi hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, milango iko wazi, mashirika na makampuni mbalimbali yapo, yanaweza yakafanya kazi hiyo ni kiasi cha Waheshimiwa kufanya mawasiliano nayo. Orodha ipo kwa yeyote atakayehitaji tutatoa copy ili aweze kujua ni kampuni gani anaweza akafanya nayo kazi. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Tatizo la ardhi kwenye Wilaya ya Mbozi linafanana sana na tatizo lililopo kwenye Mji wetu wa Tunduma. Katika Mji wa Tunduma katika Kata ya Mpemba kuna ardhi karibu ekari 500 ambazo zinamilikiwa na Shirika la Nyumba la Taifa na mpaka sasa hivi eneo lile halijaendelezwa zaidi ya miaka minane. Je, Serikali inasema nini ili kuikabidhi halmashauri, ambayo haina hata eneo la kujenga makao makuu ili iweze kutumia ardhi ile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na swali hili ambalo limekuwa kila Mheshimiwa Mbunge akiliulizia, naomba tu nitoe wito kwa Wakurugenzi wa Halmashauri pamoja na Maafisa wetu Wateule wa Ardhi popote nchini, katika maeneo na katika malalamiko ya namna hii, Sheria ya Ardhi Namba 4 ya Mwaka 1999 imewapa nguvu. Kwa hiyo, walianzishe jambo hili watuletee na sisi kama Serikali hatutawaangusha.
MHE. FRANK MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio mimi, naitwa Frank George Mwakajoka. Nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kwa kipindi hiki cha miaka miwili kumekuwa na tatizo kubwa sana la malalamiko ya wafanyabiashara katika nchi hii na wafanyabiashara wengi sana wamekuwa wakifunga biashara zao, wafanyabiashara wa maduka pamoja wafanyabiashara wa hoteli, lakini pia wawekezaji wa kutoka nje, wamekuwa wakifunga shughuli zao na kuondoka. Je, Serikali ina mpango gani wa kushughulikia malalamiko ya wafanyabiashara kuhakikisha kwamba wafanyabiashara wanaendelea kuwekeza katika nchi yetu?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme tu kwamba katika biashara yoyote ile kuna kupanda na kushuka. Kwa hiyo pamoja na kuwa tumeona kwamba baadhi ya biashara zimefungwa lakini ni ukweli pia kwamba baadhi ya biashara nyingine zimechipuka, hilo ni la kwanza. Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili mkakati wa Serikali ni kuendelea kuzungumza na wafanyabishara ili kuelewa changamoto ambazo zinawakabili, na zile ambazo zinahusu Serikali tutazitatua.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya wananchi wa Mji wa Tunduma, napenda kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wananchi wa Mji wa Tunduma wamekubali ushauri wa viongozi wao na kuondoa nyumba katika maeneo mbalimbali na kuhakisha kwamba barabara 42 zimepatikana kwenye Mji wa Tunduma, Serikali ina mpango gani wa kuwaunga mkono ili kuhakikisha kwamba barabara zile zinakuwa kwa kiwango cha lami kwenye Mji wa Tunduma, ukizingatia mji unaendelea kukua?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukulie kwamba taarifa hii ni ombi na kule wakati tunapita kwenye kampeni tulitoa ahadi zinazofanana na hayo ambayo ameyasema. Nimhakikishie tu kwamba ombi hili tutalipeleka katika timu ya wataalam ambayo ndiyo huwa inaandaa vipaumbele kulingana na ahadi za viongozi wakuu, ahadi za Wabunge, na kadhalika, waweze kuliangalia ili tuweze kulitekeleza kama ambavyo tuliahidi wakati wa uchaguzi.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kumekuwa na mkanganyiko mkubwa sana katika Halmashauri mbalimbali nchini baada ya kauli ya Mheshimiwa Rais katika sherehe za Mei Mosi juzi kule Kilimanjaro alivyosema kwamba Halmashauri yoyote au Baraza lolote la Madiwani litakalojitokeza na kutaka kumuondoa Mkurugenzi kazini au kumfukuza, Baraza hilo litavunjwa mara moja na yeye ndiye mwenye mamlaka ya kumteua Mkurugenzi kwa hiyo atahakikisha anaifuta Halmashauri hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa mujibu wa Sheria
za Serikali za Mitaa, Waheshimiwa Madiwani ndiyo wasimamizi wa shughuli na miradi ya maendeleo na mapato na matumizi ya fedha za Halmashauri.
Je, Mkurugenzi akiwa ametumia fedha vibaya na akatumia madaraka yake vibaya, ni utaratibu gani ambao Waheshimiwa Madiwani watautumia kama siyo kumuondoa Mkurugenzi wakati Rais tayari ameshawaonya na amewaambia kwamba ataivunja Halmashauri hiyo? Ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza si kweli kwamba kauli ya Mheshimiwa Rais imeleta mkanganyiko. Kauli ya Mheshimiwa Rais imemaanisha pale ambapo mkakati unafanywa na Waheshimiwa Madiwani kumuondoa Mkurugenzi kwa maslahi binafsi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uzoefu wa mwaka wangu mmoja na miezi kadhaa yote mawili yanatokea, wakati mwingine kunakuwa na mkakati wa upande wa watumishi kumuondoa Mwenyekiti na wakati mwingine kuna mkakati kwa upande wa Madiwani kumuondoa Mkurugenzi kwa sababu tu maslahi yamegongana. Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais anapolizungumzia hili hazungumzii kwa scenario unayoisema ya kwamba kumetokea ubadhirifu na wala Mheshimiwa Rais halindi wabadhirifu, anazungumzia pale ambapo kuna utaratibu unapangwa wa Madiwani kumuondoa Mkurugenzi anayesimamia watu wasifanye wizi, ndicho anachokizungumzia.
Kwa hiyo, huo mfano mwingine baki nao lakini wa
Rais ni huu aliokuwa anausema kwamba pale kunapokuwa kuna mkakati wa kumuondoa Mkurugenzi ambaye anasimamia fedha za Halmashauri hapo yuko tayari kuivunja Halmashauri na mimi mwenyewe nasema wala haitafika hata kwake mimi mwenyewe nitavunja hiyo Halmashauri.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Sera ya nchi na ya Serikali ni kuhakikisha kwamba kila kijiji na kila kitongoji kuna kuwa na zahanati, na katika mji wa Tunduma katika mtaa wa Makambini eneo la Sogea wananchi wameamua kujenga zahanati katika eneo ambalo lilikuwa limetengwa na Serikali, lakini kutokana na mgogoro uliokuwepo na ambao alikuja kuumaliza Naibu Waziri wa Ardhi, alitoa maelezo kwamba eneo hilo lisianze kujengwa mpaka atakavyotoa ruhusa ya wananchi kuendelea kujenga Zahanati pale. Je, ni lini atatoa ruhusa ili wananchi wa mji wa Tunduma eneo la Makambini waweze kuendelea na ujenzi wa zahanati kama ambavyo sera za nchi zinasema?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli nadhani Mheshimiwa Waziri wa Afya alivyopita pale wananchi waliandamana katika suala zima katika kituo kile cha afya nadhani tutafanya utaratibu kupitia ofisi yetu ya TAMISEMI nini kifanyike, lakini kutokana na changamoto ya Tunduma kwa sababu ukipita pale siku niliyopita pale population ni kubwa sana na ndio maana tunaamua kwenda kukiimarisha kituo cha Chipaka na lengo kubwa ni kwamba angalau ile kituo cha afya cha Chipaka kiweze kuwa accommodate wagonjwa wengi na tunakwenda kufanya kazi hizyo muda si mrefu ndani ya mwezi mmoja ujao kwa ajili ya wananchi wa Tanzania lengo letu ni kuboresha maeneo yale.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Serikali imekuwa ikidaiwa fedha nyingi sana na mifuko ya hifadhi, mfano, PSPF ilikuwa inaidai Serikali zaidi ya shilingi 2,671,000,000,000 pia LAPF ilikuwa inaidai Serikali zaidi ya shilingi bilioni 47 kwa ajili ya asilimia 15 ya makato kwa ajili ya wafanyakazi. Je, Serikali imelipa kiasi gani na hali ikoje kwa wastaafu hawa mpaka sasa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa Serikali ilikuwa ikidaiwa kama hiyo asilimia 15, shilingi trilioni 1.4 mpaka sasa tumeshalipa trilioni 1.1, bado shilingi bilioni tatu, ambayo mwezi huu Mei, tunakamilisha kulipa hiyo iliyobaki. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini zipo taarifa ambazo si rasmi sana kwamba zabuni ile ya kumpata mkandarasi wa kujenga daraja la Mto Momba zilisitishwa hivi karibuni na kuleta wasiwasi mkubwa sana kwa wananchi wa mikoa ya Songwe, Katavi na Rukwa kwamba daraja lao inawezekana lisijengwe. Leo Waziri anawathibitishia nini wananchi wa mikoa hiyo kwamba daraja hilo litaanza kujengwa lini?(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Wilaya ya Momba ina kanda mbili, kuna ukanda wa juu na kuna ukanda wa chini na katika Ukanda wa Chini kuna Kata za Msangano, Chitete, Chilulumo, Mkulwe, Kamsamba pamoja na Ivuna. Ukanda wa Juu kuna Kata za Kapele, Miunga Nzoka, Ikana pamoja na Ndalambo na Halmashauri ya Mji wa Tunduma. Barabara za kuingia katika Makao Makuu ya Wilaya mpya hazipitiki kabisa. Ni lini Serikali itahakikisha kwamba inatenga fedha za kujenga barabara ya kutoka Ikana mpaka Chitete na Tunduma kuelekea Chitete?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mwaka huu wa fedha wa 2016/2017 tumetenga shilingi milioni 2,935 na taratibu za kumpata mkandarasi zinazofanywa na TANROADS ziko katika hatua za mwisho. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba taratibu hizo mara zitakapokamilika, mkandarasi akipatikana atalipwa fedha hizo kama advance payment. Mwaka unaofuata ambao ujenzi utaendelea zimetengwa tena shilingi bilioni tatu kwa ajili ya kuendeleza ujenzi huo, naomba nimhakikishie hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maeneo ya barabara aliyoyataja, hayo majina kwangu ni mageni kidogo lakini kama ana maana ya ile barabara inayounganisha hii mikoa mitatu ambapo sehemu kubwa inapita eneo la Mkoa wako wa Songwe, nadhani anafahamu na mara nyingi tumekuwa tukijibu hapa kwamba mara tutakapomaliza kujenga hili daraja la Momba tutaingia sasa kwenye suala la ujenzi wa barabara. Kama ana maana ya barabara nyingine, naomba nimkaribishe ofisini tukutane na wataalam tupate ratiba ya nini hasa kitafanyika katika mwaka huu wa fedha na mwaka ujao wa fedha na hatimaye tupate majibu ya suala lake na tuweze kuwaridhisha wananchi anaowawakilisha.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kumekuwa na tafsiri ambayo siyo sahihi sana kwa vijana ambao wananunua Kwacha kwenye mpaka wa Tunduma na Zambia ambapo fedha hizo, Wazambia wanapokuwa wamekuja kununua bidhaa kwenye Mji wa Tunduma wanakuja na Kwacha na baadaye vijana wananunua zile Kwacha na Serikali imekuwa ikisema kwamba vijana wale hawalipi kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kununua zile Kwacha, wanakwenda Lusaka kununua dola na baada ya kununua zile dola wanakuja ku-change kwenye benki zetu za Tanzania. Hawa wafanyabiashara wa Kwacha wanakuwa tayari wamelipa kodi.
Je, Serikali haioni kwamba nao pia ni walipa kodi katika Taifa hili na badala yake wanaendelea kuwasumbua? Wataacha lini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, katika mipaka ambayo kuna black market ya kutisha ndani ya Taifa letu ni mpaka alioutaja wa Tunduma na ndiyo maana wiki iliyopita Mheshimiwa Waziri wa Fedha alikuwa mpakani kule na sasa tumeimarisha na tutahakikisha Mheshimiwa Mwakajoka tunakusanya kodi yote. Hawawezi kutoa Kwacha huku wakaenda kuibadilisha na wakarudi nchini bila kukusanya kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeapa kulinda na kuweza kukusanya kodi yetu, tutaikusanya kodi hii kwa kila mtu anayefanya biashara hii. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali. Dhamira ya Serikali ya kuanzisha Benki ya Kilimo ilikuwa ni kuwainua wakulima nchini. Wakati Serikali inafikiria kuanzisha Benki ya Kilimo ilikubali kutoa mtaji wa shilingi bilioni 800, lakini fedha iliyotolewa ni shilingi bilioni 60 tu na benki hii imeshindwa kabisa kuwahudumia wakulima wa nchi hii.
Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wakulima wanapata mikopo na wanalima kilimo chenye tija? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakajoka, nafikiri limekaa sawa kwa sababu linaendena hasa na jitihada ya Serikali kujaribu kuwekeza na kuwasaidia wavuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa anavyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba huko nyuma kulikuwa na jitihada kujaribu kuhakikisha kwamba Benki ya Maendeleo ya Kilimo inapata shilingi bilioni 800. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sasa benki hiyo imeweza kupata shilingi bilioni 246 tayari zimeshaingia benki na yote itaelekezwa katika kilimo ikiwa ni pamoja na kilimo cha mazao, uvuvi na ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge labda tukitoka hapa leo anione nimfahamishe taratibu za kuweza kupata hizo fedha kwa ajili ya wavuvi wake. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba hizo fedha zimepatikana.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Tunduma ni mji unaokuwa sana na una msongamano mkubwa sana wa watoto; na mwaka wa jana Waheshimiwa Madiwani kwa kushirikiana na wananchi waliweza kuanzisha shule mpya nane ambazo zingine zina madarasa matatu, zingine zina madarasa nane lakini shule hizi mpaka sasa hivi hazijaanza kutumika kwa sababu DC amewasimamisha Madiwani. Kwa, hiyo kuna baadhi ya shughuli ambazo zilitakiwa zifanyike kama vioo na mambo mengine hayajafanyika kwa sababu wananchi pia walikuwa wanategemea Madiwani. Je, ni lini Serikali itatia mkazo kuhakikisha kwamba Madiwani wanarudi kazini ili shule hizi zianze kutumika haraka iwezekanavyo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Halmashauri ilijitahidi ikajenga shule nane na hizi shule hazijaanza kutumika, ni kweli; lakini ni matokeo ya migogoro ambayo haina sababu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana wenzetu wa Halmasahuri ya Mji wa Tunduma walipokaa kwenye kikao cha rasmi walikataa ushirikiano wa aina yoyote na Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya. Sasa hilo likawa ni chanzo cha matatizo ambayo yamesababisha Waheshimiwa Madiwani wasiweze kutimiza majukumu yao. Suala lao tunalishughulikia kitaifa na namwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutalitatua hivi karibuni, ili kusudi waweze kuendelea kutekeleza majukumu yao kama kawaida. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, toka tumeanzisha Wakala wa Barabara (TARURA) katika Mkoa wa Songwe na Wilaya ya Momba hakuna barabara yoyote ambayo inajengwa sasa hivi kwenye bajeti ya mwaka 2017/2018, je, kazi hii ya TARURA itaanza kutekelezwa lini na hasa barabara ya kutoka Kakozi - Ndalambo kuelekea Kapele? Barabara ni mbaya sana na sasa haipitiki. Ahsante sana.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli na kama tunavyofahamu, ni kwamba tarehe 7 Julai, 2017 ndiyo Wakala huu umeanza kufanya kazi rasmi katika mwaka huu wa fedha tunaoendelea nao. Huu ni Wakala mpya na lengo lake ni kuhakikisha kwamba zile kazi zilizokuwa zinafanywa na Halmashauri zetu, sasa zitafanywa na Wakala huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri mwezi uliopita nilikuwa na kikao na Watendaji wote wa TARURA wa Nyanda za Juu Kusini pale Mjini Mbeya na kuwapa maelekezo mbalimbali, lakini zoezi hilo lilikuwa limekamilisha semina na maelekezo mbalimbali kwa wataalam wote wa TARURA nchi nzima. Baada ya kufanya zone zote nne, tulianza Bagamoyo tukaenda Tanga, tukaenda Mwanza na tukamalizia kule Mbeya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakala huu sasa uko katika mchakato wa stage mbalimbali. Ndiyo maana wale wanafahamu mikoa mbalimbali hivi sasa. Sasa kandarasi zinaanza kutoa mikataba kwa wakandarasi wa aina mbalimbali na mingine kutokana na zile bajeti zake zilizopita ziko kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nikuhakikishie kwamba mchakato huu unaenda na maeneo yote ya Tunduma na mikoa yote hivi sasa itashughulikiwa kwa kadri kandarasi hizo zilizotangazwa. Naomba niwahakikishie kwamba katika hili hatutakuwa na masihara katika usimamizi hasa wa ukandarasi utakaofanyika kule site, lengo letu ni kwamba Halmashauri zipate barabara bora kwa lengo kubwa la kuwasaidia wananchi wetu.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Matatizo ya usalama katika eneo la Bunda yanafanana sana na Jimbo langu la Mji wa Tunduma.
Mwaka 2016 katika swali langu la msingi, niliuliza kuhusiana na ujenzi wa kituo chenye hadhi ya Wilaya, lakini pia niliuliza kuhusiana na nyumba zenye gharama nafuu kwa ajili ya polisi wetu kwenye Mji wa Tunduma. Majibu yake ni kwamba walisema katika Bajeti ya mwaka 2016/2017 nyumba hizi zingeweza kujengwa pamoja na Kituo cha Polisi chenye hadhi ya Wilaya. Je, Serikali inasema nini kuhusiana na changamoto hizi katika mji wetu wa Tunduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nakiri kabisa kwamba Jimbo la Tunduma lipo mpakani na lina changamoto nyingi sana za kiusalama. Kwa hiyo, mahitaji ya kuwa na kituo cha polisi cha kisasa pamoja na nyumba za askari ni mambo ya kipaumbele.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi hiyo iliyotolewa na Serikali iko pale pale na hatua ambazo zitafikiwa tutamjulisha kwa kadri ambavyo upatikanaji wa fedha utakavyokuwa unaruhusu.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri, naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli mbiu ya Serikali sasa ni viwanda, lakini viwanda havitakuwepo katika nchi hii kama hatutoweza kuzalisha mafundi mchundo wengi ili waweze kutekeleza majukumu mbalimbali ndani ya viwanda hivyo. Je, Serikali haioni kwamba inapoteza muda wa kutamka kwamba itakuwa ni Serikali ya viwanda wakati haitaki kuzalisha mafundi mchundo wengi ili waweze kutekeleza wajibu wao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika hali halisi
ya majibu ya Mheshimiwa Waziri jana wakati anajibu hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge alisema kwamba Serikali imejipanga kujenga Vyuo vya VETA nchi nzima na maeneo mbalimbali katika Taifa hili. Leo katika majibu yake anatuambia kwamba Serikali haina mpango wa kujenga Chuo cha VETA katika Mji wa Tunduma. Je, jana alikuwa akiwadanganya Wabunge katika majibu yake ya msingi aliyokuwa akiyatoa ndani ya Bunge hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi Serikali inatambua juu ya umuhimu huo wa kuendelea kuzalisha mafundi sanifu na mafundi mchundo pamoja na wahandisi, lakini njia za kuzalisha mafundi hao haziko tu kupitia VETA, zipo pia kupitia vyuo binafsi lakini pia kupitia mafunzo ya muda mfupi ambayo wanafundishwa na kuweza hata kujitegemea katika viwanda vidogo vidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huo upo, kwa mfano mwaka huu, kuna mafunzo ya vijana wapatao 23,000 ambayo yanaendeshwa na VETA ambayo ipo chini ya Wizara yetu lakini pia kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Ajira, Vijana na watu Wenye Ulemavu kuhakikisha kwamba vijana wengi wanapata fursa hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusiana na majibu yangu kwamba jana nimesema tutajenga vyuo nchi nzima. Kwanza naomba nipende kuliomba Bunge lako Tukufu, naona kuanzia jana hiyo kama ulivyosema na pengine siku zote Waheshimiwa Wabunge pengine huwa hawanisikilizi vizuri ninapotoa majibu yangu kiasi kwamba wameanza kuniwekea maneno ambayo sijazungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema ni hivi Serikali ina dhamira ya kujenga Vyuo vya VETA katika kila Wilaya lakini vilevile kuhakikisha kwamba inaimarisha Vyuo vya Wananchi kila mahali vilipo ambapo vipo 55. Hata hivyo, kwa sasa kutokana na hali halisi ya kibajeti tumesema tutaimarisha kwanza vyuo vilivyopo na vile ambavyo vilishakuwa vimeanza mchakato wa kuanza kuvijenga. Kwa hiyo, sio kwamba tutajenga tu kila mahali bila utaratibu au bila fedha, naomba nieleweke hivyo tafadhali. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Mji wa Tunduma uko mpakani mwa Zambia na Tanzania na ni Mji ambao unahudumia Mataifa zaidi ya Nane yanaotumia Mpaka wa Tunduma, lakini kumekuwa na tatizo kubwa sana la umeme kukatika mara kwa mara na kusababisha usalama wa wageni pamoja na Wakazi wa Mji wa Tunduma kuwa hatarini. Je, ni lini Serikali itaweka umeme wa uhakika, kama ambavyo wenzetu wa Zambia pale ng’ambo walivyoweka umeme wa uhakika? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii na napenda nimshukuru Mheshimiwa Frank kwa swali lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme Wilaya ya Tunduma ipo katika Mkoa wa Songwe, Mkoa ambao awali ulikuwa Mkoa mmoja wa Mbeya, kwa hiyo line zote zinazopeleka umeme katika Mkoa mpya wa Songwe zinatokana na Mkoa wa Mbeya. Kwa hiyo ni wazi njia ndefu ya kupeleka umeme katika Mkoa wa Songwe inasababisha kukatikakatika kwa umeme katika maeneo mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali kwa sasa pia ni kujenga Sub Station kubwa Tunduma ili kuwezesha upatikanaji wa umeme vizuri. Kwa sasa pia kuna mpango wa kujenga line ya kV 400 ambayo inaanzia maeneo ya Tunduma mpaka Mbeya inaenda mpaka Sumbawanga kwa ajili ya kurahisisha usafirishaji wa umeme katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge Serikali ya Awamu ya Tano inatambua hilo tatizo, lakini mipango hii ipo na itatekelezeka na baada ya muda umeme utakuwa ume-stabilize katika Mkoa Mpya wa Songwe. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Tunduma na Wilaya yetu ya Momba kulikuwa na majengo ambayo yalikuwa yanatumika na Kampuni ya CC iliyokuwa inajenga barabara ya kutoka Tunduma kwenda Sumbawanga. Majengo hayo yaliteuliwa kwamba yangeweza kutumika kama Hospitali ya Wilaya, lakini sasa hivi inaonesha kuna mabadiliko. Waziri anawaambia nini wananchi wa Mji wa Tunduma kuhusiana na majengo yale kwa sababu aliwahakikishia kwamba itakuwa Hospitali ya Wilaya?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza nitaenda kufanya follow up kujua kwamba ni Waziri gani alitoa commitment hiyo.
Jambo la pili, nafahamu wazi kwamba kuna maeneo mengi sana majengo yaliyokuwa yakitumika na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi, hasa yale makampuni, majengo yale mengi sana yameombwa kwa ajili ya ama vituo vya afya au maendelezo ya Hospitali za Wilaya. Ninafahamu wazi kwamba Tunduma kuna changamoto kubwa kwa sababu idadi ya watu pale ni kubwa na ndiyo maana tunaanza ule ujenzi wa kituo cha afya, japokuwa umekuwa ukisuasua lakini tutasimamia kwa karibu ili uweze kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo hilo ndugu yangu Mheshimiwa Mwakajoka naomba niseme kwamba tunalichukua kwenda kulifanyia tathmini kuona nini kimekwamisha, kwa sababu hatimaye tunataka wananchi wa Tunduma wapate huduma vyema kabisa. Kwa hiyo tutalifanyia kazi Serikali kwa ujumla wake wote.
MHE. FRANK. G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mji wa Tunduma una shida kubwa sana ya maji na mwaka jana katika bajeti ya mwaka 2016/2017 ilikuwa imetengwa fedha Euro milioni 100 ambayo ilitaka kutekelezwa na Kampuni ya Aspac International kutoka Ubelgiji, lakini katika bajeti hii fedha hiyo haijatengwa na mradi huo hauonekani kabisa. Nataka nijue mradi wa kupunguza tatizo la maji katika Mji wa Tunduma utatekelezwa siku gani na kwa nini umeondolewa hauonekani katika bajeti ya mwaka 2017/2018?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba Serikali imepanga kukopa fedha kutoka Ubelgiji. Mazungumzo yanaendelea kati ya Hazina na Serikali ya Ubelgiji kupitia Benki hiyo ambayo imeonesha nia ya kutuazima hiyo fedha. Kwa hiyo mazungumzo yakishakamilika, basi huo mradi utaendelea, anashangaa kwa nini haujaonekana katika mwaka ujao wa fedha ni kwa sababu mazungumzo hayajakamilika Mheshimiwa Mbunge. Hata hivyo, nimhakikishie sasa hivi nazunguka kwenye Miji yetu ya mipakani nchi nzima. Namwahidi kwamba ninapokwenda nyumbani nitapita Tunduma lazima tufanye hatua za dharura kama nilivyofanya Namanga na maeneo mengine ili wananchi wapate maji safi na salama pale Tunduma.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kabla sijauliza swali la nyongeza ningependa nitumie fursa hii kuishukuru sana Serikali ya Zambia kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya ya kuhakikisha kwamba wanatuazima gari yao ya Zimamoto kwa ajili ya kuzima moto kwenye mji wa Tunduma, ninasema mwasalifya sana mwe wantu wa Kuzambia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza; najua kabisa kwamba Tunduma iko mpakani mwa Zambia na Tanzania na shehena kubwa sana ya mizigo inayoshuka kwenye bandari ya Dar es Salaam inapita Tunduma na Tunduma hatuna gari ya Zimamoto. Je, Serikali haioni kwamba inahatarisha maisha ya wana Tunduma lakini pia na mizigo inayopita kwenye mpaka wa Tunduma?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, wananchi wa Tunduma wanaendelea kutoa ada za zimamoto wakati huduma ya zimamoto kwenye Mji wa Tunduma haipo, hatuoni kama huu ni uzulumaji wa wazi kabisa wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa wananchi wa Tunduma kuendelea kutozwa fedha hizi bila kupata huduma ambayo ni muhimu katika maisha yao? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Spika, kwanza alivyotoa shukurani hizi nikapata mashaka sana, maana mipakani kule kuna mwingiliano sana wa uraia na nilipoona sifa nyingi sana zinaenda Zambia nikataka kujua sana babu zake wake wako wapi. (Makofi/Vicheko)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Spika, lakini yote kwa yote ni kheri. Niseme tu kwamba yale aliyoyasema Mheshimiwa Mwakajoka kwa utaratibu wetu, tungekuwa hatuna gari kabisa katika eneo husika ingekuwa ni hatari sana, lakini vitu hivi vya moto huwa vinaharibika, na kama nilivyosema kimeenda matengenezo na baada ya hapo kitarudi.
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu kuwatoza hii ni kwa mujibu wa sheria na sheria za kodi za nchi yetu, si kila kodi inakwenda specific huduma kwa mtu aliyechangia kodi hiyo, na tukifanya hivyo tutakuwa tumekosea kwa sababu kuna maeneo mengine makusanyo ni kidogo.
Kwa hiyo, mimi nitoe rai kwa wananchi wetu waendelee kutoa kodi hizo na hivi tunavyoongea kwenye bajeti iliyopita tumepitisha bajeti ya magari mengine, tunategemea kupata magari mengine kwa ajili ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na huduma hiyo itasambaa katika maeneo mengi zaidi kama ambavyo tumepanga katika malengo yetu. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Katika Bunge lililopita niliuliza swali kuhusiana na hospitali ya wilaya ambayo tulikuwa tumeambiwa kwamba itajengwa katika Kata ya Chipaka kwenye Kijiji cha Chipaka. Sasa hivi inaonesha kwamba kuna mabadiliko ambayo yanataka kufanyika hospitali ile ikajengwe maeneo mengine ambayo hayana majengo kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo tulilokuwa tumeliteua ni eneo ambalo lilikuwa na majengo ambayo yalikuwa yanatumika kwa ajili ya mradi wa kujenga barabara kutoka Tunduma kwenda Sumbawanga, kuna majengo zaidi ya 20, leo hii wanataka kupeleka maeneo ambayo hayana majengo kabisa. Mheshimiwa Waziri aliniambia hapa atahakikisha kwamba analifuatilia jambo hili na hospitali inajengwa eneo ambalo walikuwa wametuambia kwamba ni lazima itajengwa pale. Je, amefuatilia na anatoa majibu gani kwa wananchi wa Tunduma ili wawe na uhakika wa hospitali katika eneo la Chipaka na Kata ya Chipaka? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la nyongeza la Mheshimiwa Marwa nimeeleza kwamba ramani kwa ajili ya hospitali za wilaya ambazo zimekuwa designed na Ofisi ya Rais, TAMISEMI zinajitosheleza. Katika pesa ambazo tunakwenda kuanzia tunakwenda kuanza na jumla ya shilingi bilioni 1.5 kwa ramani ambayo ni sahihi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa asingependa tukaenda kwenye majengo ambayo hayakidhi ramani ambazo tunazo, ni vizuri tukapeana nafasi na naamini na yeye mwenyewe akiona ramani pendekezwa ataafiki kwamba ni vizuri majengo yale yakatafutiwa kazi nyingine, lakini sisi tungependa tujenge hospitali ya wilaya yenye hadhi ya kulingana na Mheshimiwa Mbunge ambaye anatoka Tunduma.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa kigezo cha kutoa asilimia 0.3 kwenye Halmashauri ambazo kuna kazi za uchimbaji unaofanywa na migodi inatokana na athari ambazo wananchi wa maeneo hayo wanapata. Katika Mji wa Tunduma kuna forodha ambayo inahudumia nchi karibu nane Kusini na Kati mwa Afrika na kumekuwa na madhara mengi sana kwenye mpaka wa Tunduma ambayo yanafanana kabisa na maeneo wanayochimba migodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, kuna magonjwa ya UKIMWI lakini kuna miongamano mkubwa sana wa magari na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi wangu ambao wanashindwa kutekeleza majukumu yao ya kimaendeleo vizuri.
Je, Serikali haioni kwamba sasa ni muda muafaka kuona na sisi kama Halmashauri ya Tunduma tunaweza kupata asilimia 0.3 ya ruzuku kama ambavyo wanapata katika maeneo ambayo wanachimba migodi? Ahsante.
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri na nipende kujibu swali la Mheshimiwa Mwakajoka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa kama ambavyo kifungu cha 6(1)(u) cha Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa kinavyoeleza, fedha hii ya ushuru wa huduma si kwa ajili ya madhara ni kwa ajili ya wao kupata stahiki ya huduma mbalimbali na mapato yaliyotokana na shughuli za uchimbaji. Kama ambavyo tumeeleza, kwa upande wa Tunduma bado hakuna leseni ya uchimbaji madini ambayo ilitolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa ufuatiliaji tumekuwa makini kufuatilia kutaka kujua kwa nini Mheshimiwa Mbunge amekuwa akitaka kuulizia suala hili. Tumefuatilia katika eneo la Mkombozi na Chapwa ambapo katika eneo la Chapwa kulikuwa na shughuli za uchimbaji wa madini ya ujenzi ya kifusi, lakini yalikuwa yakichimbwa kwa ajili ya upanuzi wa barabara. Kwa sasa tunachokifanya tumeanza kurasimisha ili leseni ziweze kutolewa kwa wale ambao waliokuwa wakichimba kwa kificho basi waweze kuingia katika shughuli hizo za uchimbaji kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu na waweze kugaiwa leseni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asubiri tu, leseni zitakaporasimishwa kwa wachimbaji wale katika eneo la Chapwa pamoja eneo la Mkombozi basi wataweza kupata ushuru huu wa huduma au service levy.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, reli ya TAZARA ni reli ambayo ingeweza kusaidia sana kusafirisha mizigo kutoka Dar es Salaam na kupeleka nchi za Congo, Zambia na Zimbabwe na kuepusha uharibufu mkubwa wa barabara ambao umekuwa ukitokea kutoka Dar es Salaam kwenda Tunduma. Tumeshangaa kwamba mizigo mingi wanatumia malori kusafirisha badala ya reli ya TAZARA. Je, kuna changamoto gani ambazo Serikali imezigundua kutokana na wafanyabiashara wengi kutokutumia reli hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, reli yetu ya TAZARA imekuwa ikifanyakazi kwa muda mrefu sana na imekuwa ikihudumia mizigo pamoja na abiria kutoka Dar es Salaam mpaka Kapirimposhi nchini Zambia na kusema kweli Shirika letu hilo la TAZARA limekuwa likifanyakazi nzuri sana katika huduma hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hivi karibuni kumejitokeza baadhi ya wafanyakazi wasiokuwa waaminifu ambao walikuwa wanaishauri vibaya Serikali kitendo kilichosababisha sasa tuanze kukosa mizigo kutoka kwa wateja wetu ambao ni muhimu sana ikiwemo kile kiwanda cha kutengeneza saruji ambacho kiko Mbeya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hivi karibuni nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Serikali imekwishalifanyia kazi na kuna timu ya wataalam inafuatilia kuhakikisha wateja wetu wote ambao walipotea wanarudishwa. Na sasa hivi nimhakikishie tu Mheshimiwa Mwakajoka kwamba wateja wale wakubwa tumekwishaanza kuwarudisha na TAZARA sasa inafanyakazi nzuri sana. Tuna uhakika ndani ya mwaka mmoja huu wateja wote watakuwa wamesharudi kwa sababau hakuna njia nyepesi na nzuri na salama ya kusafirisha mizigo na abiria kama reli zetu kupitia TAZARA na TRC.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uko mradi ambao unataka kutekelezwa kwenye Mji wa Tunduma na SADC na Mheshimiwa Waziri katika Bunge lililopita alisema kwamba ameshampeleka consultant pale. Wananchi wa Tunduma wanataka kujua mpaka sasa mradi umefikia kiwango gani katika maandalizi ya utekelezaji?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli consultant ameenda kwa ajili ya mradi huo lakini taratibu za utekelezaji zinakwenda hatua kwa hatua. Kwanza consultant anakwenda kufanya study analeta hiyo study tutaipitia baadaye kama pesa ipo utafuata mchakato wa kutafuta mkandarasi ili aweze kufanya kazi hiyo.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Kuna mpango wa kujenga mradi mkubwa wa maji ambao unatakiwa kutekelezwa na SADC katika Mji wa Tunduma pamoja na Mji wa Nakonde upande wa Zambia. Ni nini mkakati na Serikali imefikia wapi katika kujenga mradi huu mpaka sasa?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, tayari Serikali ya Chama cha Mapinduzi inatekeleza mradi wa muda mfupi, imechimba visima viwili pale Mjini Tunduma, imeweka pump na juzi nilienda kule kwenda kuangalia. Changamoto ni kwa kisima kimoja ambacho waliweka bomba lenye diameter ndogo, kwa hiyo, maji yakawa hayatoki kwa wingi, lakini na matenki tumeshajenga, tumetoa maelekezo tunaboresha hiyo huduma.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na mradi mkubwa wa Tunduma/Nakonde, tayari consultant ameanza kazi ya kufanya feasibility study. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asiwe na wasiwasi tutatekeleza huo mradi kwa ajili ya Tunduma kwa upande wa Tanzania na Nakonde kwa upande wa Zambia na hasa kwa sababu chanzo cha maji kinatoka upande wa Zambia.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kumekuwa na mkanganyiko mkubwa sana katika Deni hili la Taifa, Wabunge wamekuwa wakihoji sana kwamba deni limekuwa kubwa na wanahoji pia kwamba Serikali imekuwa ikikopa fedha na kulipia kwenye madeni ambayo tumekopa katika maeneo mengine. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuleta sheria ndani ya Bunge ili fedha yoyote inayokopwa na Serikali itakiwe kuidhinishwa ndani ya Bunge kwamba sasa Serikali ikope? Siyo Serikali inakopa tu halafu baadaye kunakuwa na hoja ambazo zinaleta mkanganyiko ndani Bunge hili na kwa Watanzania pia wanashindwa kujua fedha hizi zimefanya kazi gani. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Frank, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kama nilivyomjibu Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Serikali hukopa baada ya Bunge lako Tukufu kupitisha kiwango kilichoombwa na Serikali kuhusu ukopaji huo na nimetaja sheria inayosimamia haya yote tunayoyatenda. Napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba katika kipindi ambacho Serikali yetu ilitakiwa kupongezwa ni kipindi cha Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa sababu tumeimarisha makusanyo ya mapato yetu ya ndani na tunalipa deni letu kupitia makusanyo ya mapato yetu ya ndani.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri yanayotoa faraja kwa wananchi wa Tunduma pamoja na Ileje, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, wananchi wa Kata ya Bupigu, Kata ya Malangali, Kata ya Isoko na Kata ya Ikinga katika Wilaya ya Ileje wamekuwa na adha kubwa sana ya kuamka Saa nane ya usiku na kusubiri usafiri kuja makao makuu ya Mkoa wa Songwe. Ni lini Serikali itajenga barabara hii ya kutoka Isongole mpaka Ikinga, ili kuondoa adha hii ya Wananchi wa Ileje?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuna kipande cha barabara kilometa 1.6 kimejengwa katika Mji wa Tunduma na kimejengwa kwa sababu, wananchi wa Mji wa Tunduma wakati Mheshimiwa Rais akiwa Waziri wa Ujenzi, wakati anapita anakwenda Rukwa, walimsimamisha pale na wakamwomba barabara ile ijengwe haraka iwezekanavyo na sasa Serikali imejenga kipande kile cha kilometa 1.6, lakini kipande kile kimejengwa chini ya kiwango. Je, ni lini Serikali itakuja kuhakiki kipande kile cha barabara ili wananchi wa Tunduma waweze kufurahia mpango wa ujenzi wa barabara kwenye Mji wa Tunduma?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kama anavyouliza, anapenda kujua katika swali lake la kwanza, katika hizi Kata za Lupingu, Malangali na Ikinga, kuna sehemu ambayo ina uharibifu mkubwa, kwamba, kwa kweli, maeneo mengi tumekuwa na uharibifu kutokana na mvua zimekuwa nyingi, lakini kama tulivyopitishiwa bajeti na Bunge lako, tumetenga fedha kwa ajili ya kufanya matengenezo, ili kuhakikisha kwamba, maeneo haya yanapitika.
Mheshimiwa Spika, kabla hatujapata kipande cha lami katika eneo hili nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Tunduma kwa ujumla kwamba wakati hizi mvua zinapungua tumejipanga kwa ajili ya kufanya marekebisho makubwa ili maeneo haya yapitike. Kwa hiyo, nimtoe tu wasiwasi kwamba tutafanya marekebisho ili wananchi waendelee kupata huduma ili waondokane na hii adha ambayo wanaipata.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, kuhusu kile kipande cha kilomita 1.6 ambacho Mheshimiwa Mbunge anaona kwamba hakikujengwa katika standard inayotakiwa; niseme tu kwa sababu nitakuwa na ziara ya maeneo yale kwamba tutayaona kwa pamoja ili tuone kwamba hii kilomita 1.6 ina shida gani ili tuone kama kweli ni kiwango hakikuwa kimefikiwa au labda saa nyingine ndiyo ilikuwa kuna shida tofauti ya hapo kwa sababu kuna wakati mwingine barabara zinajengwa lakini mazingira ambayo hayakutegemewa yanaweza yakatokea barabara ikaharibika.
Mheshimiwa Spika, tutaiona kwa pamoja na Mheshimiwa Mbunge halafu tuone tutachukua hatua kama kutakuwa na shida yoyote kuhusu kipande hiki ambacho umekitaja.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vijana wengi sana pale Tunduma wamejiajiri kwa ajili ya kufanya escort ya magari yaliyobeba copper kutoka Congo na wamefanya kazi kwa muda mrefu lakini mpaka sasa hivi hawajapata mikataba kutoka kwenye kampuni hizo. Serikali inasema nini kuhusiana na vijana hao kwa sababu imeonesha kwamba kampuni hizo zinavunja sheria; kwa sababu wamefanya miaka mitatu wengine mpaka miaka nne lakini mpaka leo hawana mikataba kabisa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Frank Mwakajoka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria Namba 6 ya Mwaka 2004, kifungu cha 14 kimetoa sharti la kila mfanyakazi kupewa mkataba. Kama vijana hawa wanaofanya kazi Tunduma hawana mkataba maana yake waajiri wamevunja sheria. Natoa maelekezo kwa Afisa Kazi wa Mkoa wa Songwe kuhakikisha kwamba anakwenda kufanya ukaguzi katika eneo hilo na taarifa itakayotoka tutaifanyia kazi ili vijana hao waweze kupata mikataba ya ajira.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mji wa Tunduma ni wa kibiashara na kuna mpaka ambao unatumiwa na nchi karibu nane za Kusini na Kati mwa Afrika. Kumekuwa na msongamano mkubwa sana wa malori yanayovuka mpaka ule na kusababisha wananchi wa Tunduma kuchelewa kufanya shughuli zao kwa sababu ya msongamano ule. Kuna barabara ya kilometa 12 kutoka eneo la Mpemba kuja Tunduma Transfoma ambapo viongozi wengi wameahidi kuijenga kwa kiwango cha lami ili kupunguza msongamano kwa magari yanayotoka Sumbawanga kwenda Mbeya na yanayotoka Mbeya kwenda Sumbawanga lakini pia kuwarahisishia usafiri wananchi wa Mji wa Tunduma. Je, ni lini Serikali itajenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami kama ahadi za viongozi zilivyotolewa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakajoka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua ziko challenge kubwa za msongamano wa magari kwa sababu Mji wa Tunduma unakua kwa kasi na huduma za kijamii zimeongezeka sana. Nimhakikishie Mheshimiwa Mwakajoka na wananchi wa Tunduma kwamba tumejipanga vizuri kuhakikisha maeneo yote ambayo yana changamoto za msongamano tunayashughulikia, kwa hiyo, nimtoe hofu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sijafanya ziara Mkoa wa Songwe, baada ya Bunge hili nitatembelea huko, nafikiri itatupa nafasi zaidi tuweze kuzungumza na niweze kuona. Pia niione mipango iliyoko TANROADS Mkoa kuhusu maboresho ya eneo hili la Tunduma ili tuweze kuondoa shida ambazo zinawapata wananchi na kuondoa tatizo la kupoteza muda kwa ajili ya kwenda kuzalisha katika maeneo mbalimbali.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Tunduma uko mpakani mwa Zambia na Tanzania na ni mji ambao unapokea wageni wengi wanaotoka nchi za Kusini mwa Afrika lakini huduma ya umeme kwenye Mji wa Tunduma ni haba sana na umeme unakatikakatika mara kwa mara na kusababisha usalama wa wageni na wananchi wa Tunduma kuwa hatarini. Je, ni lini Serikali itahakikisha kwamba inaweka umeme wa uhakika katika Mji wa Tunduma?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tukushukuru sana kwa namna ambavyo umetambua mahitaji ya nishati na kuwapa fursa Waheshimiwa Wabunge kuuliza maswali mengi. Umenipa fursa ya kujibu maswali ya Mheshimiwa Njeza, Mheshimiwa Mwamoto pamoja na Mheshimiwa Frank.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Njeza na Mheshimiwa Mwamoto maswali yao yanalingana kwa sababu yamehusisha masuala ya umeme vijijini. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Njeza, tulifanya ziara Mbeya, pamoja na kwamba Jimbo lake ni Mbeya Vijijini, hapa amezisemea kata ambazo zipo ndani ya Jiji la Mbeya, na kama nilivyosema, Serikali imetambua ukuaji wa maeneo katika Miji, Manispaa na Majiji na ndiyo maana tumekuja na mradi huu unaoitwa Peri-Urban. Niliombe Bunge lako tukufu, tutakapowasilisha bajeti yetu ya mwaka 2018/2019 ituunge mkono katika miradi mbalimbali ukiwemo Mradi huu wa Peri- Urban kuupitisha kwa kishindo kisha tufanye kazi ya kupeleka umeme katika maeneo ambayo hayajafikiwa na huduma hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo, Mheshimiwa Mwamoto, ni kweli tulifanya ziara tena kwa mara ya kwanza Mawaziri wawili, Mheshimiwa Waziri mwenyewe na mimi Naibu Waziri tulikuwa kwenye kata hiyo aliyoitaja. Nataka niseme sisi lengo letu ni kupeleka nishati kwenye maeneo yenye uhitaji ikiwemo mojawapo ya maeneo ambayo kweli yanahitaji nishati ni eneo la viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwapongeze Mheshimiwa Mbunge na vijana hao kwa kutenga eneo la viwanda vidogo vidogo na kwa gharama za Serikali umeme utafika katika maeneo hayo na nitoe rai tu wao waendelee kujipanga kuunganisha lakini umeme utafika kama ambavyo tumeahidi katika ule mkutano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la mwisho la Mheshimiwa Frank, ni kweli Mji wa Tunduma ni mji ambao umekuwa na upo mpakani. Nataka niseme Mji wa Tunduma upo katika Mkoa mpya wa Songwe na wakati huo umeme katika Mkoa wa Songwe ulikuwa unatoka katika njia ya kusafirisha umeme ni ndefu kutoka Mbeya. Serikali ina mpango wa kujenga sub-station palepale Tunduma kwa ajili ya kuufanya Mkoa mzima wa Songwe upate nishati ya uhakika na wakati wote. Kwa hiyo, nimthibitishe Mjumbe kwa kuwa yeye Mheshimiwa Mbunge ni Mjumbe wa Kamati yetu ya Nishati na yeye pia atuunge mkono katika bajeti yetu ili mradi huu wa ujenzi wa sub-station pamoja na line ambayo inatoka Mbeya inayoenda Sumbawanga - Mpanda – Kigoma - Nyakanazi ya KV 400 ambayo yote kwa pamoja itachangia kwa upatikanaji wa umeme wa uhakika. Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, ahsante sana.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nilikuwa nataka nipate ufafanuzi kutoka kwa Mheshimiwa Waziri. Wanatumia kigezo gani katika kupanga ushuru wa dagaa hasa dagaa zinazotokea bahari ya Hindi? Wafanyabiashara walikuwa wanalipwa kwa gunia la kilo 100 shilingi 10,000/=, lakini sasa hivi kilo moja wanalipisha dola moja. Kwa hiyo, gunia hilo sasa hivi limefika mpaka shilingi 250,000/=. Wafanyabiashara wameshindwa kufanya biashara hiyo. Serikali inasema nini kuhusiana na jambo hilo kwa sababu linaathiri biashara katika mpaka wa Tunduma? Ahsante.
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Mwakajoka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake. Vigezo vya kupanga ushuru wa dagaa au wa bidhaa au wa mazao yoyote ya uvuvi, hutegemeana na thamani ya zao lenyewe linalohusika. Kwa hiyo, hiyo ndiyo hasa zana yake, thamani yake ili Taifa liweze kunufaika na mazao yake hasa yanapotokea kuuzwa nje. Kwa hiyo, kama kuna shida yoyote ambayo katika kubadilisha tozo aidha, zimeweza kuleta mkwamo mkubwa wa biashara, sisi tutatathmini, tutaangalia. Mheshimiwa Mbunge, kama hilo limeleta shida, tutaangalia kwa sababu sasa hivi tunaingilia tunaanza kuzitazama tozo zetu upya kama unavyojua tunaingia kwenye bajeti, kama kuna mahali itaonekena tozo hizi zimewekwa kubwa sana kuliko biashara ilivyo, tutazipunguza na hilo halina matatizo yoyote.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la MKUKUTA na Ilani ya Chama cha Mapinduzi sekta ya kilimo ilikuwa ikue kwa asilimia 8 ndani ya miaka 10 lakini uhalisia kuanzia mwaka 2011 na 2015 sekta ya kilimo ilikua kwa asilimia 3.4. Ndani ya miaka ya Awamu ya Tano katika miaka yake mitatu ya bajeti sekta ya kilimo imekua kwa wastani wa asilimia 1.9. Uhalisia unajionesha kwenye bajeti zake, bajeti ya mwaka 2016/ 2017…

MWENYEKITI: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016/2017 tulitenga shilingi bilioni 101 katika sekta ya kilimo lakini fedha iliyotoka ilikuwa ni shilingi bilioni 3 peke yake. Pia mwaka 2017/2018 tulitenga shilingi bilioni 150 ikatoka shilingi bilioni 24. Swali, hii ndiyo tafsiri ya Kilimo ni Uti wa Mgongo katika Taifa letu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wote tunajua kwamba Watanzania wengi wanaohitimu vyuo vikuu katika Taifa hili ni 800,000 lakini watu ambao wanaajiriwa kwenye sekta rasmi karibu watu 20,000 tu ambapo 780,000 wanakwenda kuajiriwa kwenye sekta ya kilimo. Hata hivyo, sekta ya kilimo kumekuwa na tatizo la uwekezaji, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba wahitimu hawa wanapewa mikopo ili wajiajiri na wainue maisha yao pamoja na kuchangia pato la Taifa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mwakajoka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza Mheshimiwa Mwakajoka anasema kwamba sekta ya kilimo imekua ikikua kwa asilimia ndogo kinyume na matarajio. Pamoja na mipango mizuri ya Serikali katika kukuza sekta ya kilimo nchini lakini kuna mabadiliko ya tabianchi ambayo yanaathiri productivity ya kilimo nchini. Hata hivyo, Serikali inayo mipango madhubuti kupitia Mpango wa Kilimo wa ASDP II kama nilivyotaja kwenye majibu yangu ya msingi, kuhakikisha tunatumia ardhi vizuri kwa kilimo, tunazingatia matumizi mazuri ya utumiaji wa maji ili kwenda kwenye kilimo cha umwagiliaji yaani drip irrigation pamoja na mikakati mingine ambayo tumeiweka ndani ya Serikali kupitia Mpango huu wa Maendeleo ya Kilimo wa ASDP II.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili la Mheshimiwa Mwakajoka ni kwamba tuna vijana wengi ambao wanahitimu kwenye vyuo vikuu lakini kuna changamoto ya ajira; na wanaoenda kwenye kuajiriwa kwenye sekta ya kilimo ni wachache, asilimia ni ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali katika hili ni kuhakikisha tunaleta mageuzi ya kilimo na kufungamanisha kilimo na viwanda. Kama unavyojua Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge, Serikali inaendelea kufanya jitihada hizi kuangalia kilimo kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, asilimia 65 ya malighafi za viwandani zinategemea mazao yetu ya kilimo. Sasa mkakati wa Serikali ni kuongeza hizi asilimia ili tuweze kufungamanisha uchumi wa viwanda na kilimo.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Migogoro ya ardhi katika nchi hii ipo katika kila wilaya na kila mkoa, lakini katika Mkoa wetu wa Songwe mpaka sasa hivi hatujapata Baraza la Ardhi la Wilaya na Wilaya zetu za Ileje Momba na maeneo mengine zinakwenda Mbeya Mjini. Je,ni lini Serikali sasa itaanzisha Baraza la Ardhi la Wilaya katika Mkoa wetu wa Songwe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Meshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakajoka kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ambayo Serikali inatakiwa kufanya kazi kila wilaya inapaswa kuwa na Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya na tayari tulishasema na kutoa majibu tuna mabaraza 97 ambayo tayari yalikwishaanzishwa na sasa hivi yote yatakwenda kufanya kazi kwa maana ya kwamba tumepata baadhi ya watumishi ambao wanakwenda. Hata hivyo, kufungua Baraza la Ardhi katika eneo inategemeana pia na idadi ya kesi na namna ambavyo wilaya yenyewe imejiandaa katika kutupa ofisi, kwa sababu katika maeneo ambayo tunafanyia kazi hiyo, Wizara haijengi ofisi bali Halmashauri na mkoa husika wanatupa majengo, sisi tunapeleka watumishi pamoja na vitendea kazi, kwa maana ya thamani. Kwahiyo kama watakuwa tayari, basi tunaweza tukafika katika eneo hilo, lakini pia tunazingatia takwimu na migogoro iliyopo. Ahsante.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kila mwananchi wa Tanzania ana haki ya kulindwa na Serikali yake na sasa hivi kumetokea wimbi kubwa sana kwenye Nchi ya Afrika Kusini, wageni wanauawa, wanatekwa, wanachomwa moto na wanateswa sana. Je, Serikali ya Tanzania imechukua hatua gani kuwalinda Watanzania wote ambao wako Nchini Afrika Kusini kwa kipindi hiki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulivyosema, suala hilo ni la Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Ni suala ambalo limekuja mahali pasipokuwa pake kwa sababu bado ipo siku ya bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na linaweza kuwa ni swali ambalo linajitegemea. Hata hivyo, msizoze, acha kuzoza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwanza ninapenda kusema kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Afrika ya Kusini zina mahusiano mazuri sana ya kindugu na ya muda mrefu. Ndiyo maana nichukue fursa hii pia kumpongeza Cyril Ramaphosa kuchaguliwa kuwa Rais wa Afrika Kusini; na inshallah tukijaliwa tutahudhuria kuapishwa kwake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la usalama wa Watanzania siyo wa Afrika ya Kusini tu, usalama wa raia wa Tanzania popote walipo ni jukumu la Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kuhakikisha Watanzania popote walipo wapo salama. Kwa hiyo, suala hilo linafuatiliwa na Serikali ya Afrika Kusini yenyewe imeziandikia Nchi zote za Afrika; moja, kuomba radhi kwa yale yote yanayotokea nchini mwao ambayo yanaonekana kuwa ni ya ubaguzi na yanayoifanya Afrika ya Kusini ionekane ni nchi ambayo haikumbuki ilivyosaidiwa na Waafrika wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali ya Afrika ya Kusini yenyewe imetuletea andiko kupitia Ofisi ya Ubalozi kuomba radhi kwa yale ambayo yanatokea. Nasi tunachukua hatua moja ya kuhakikisha raia wote waliko Afrika Kusini wako salama; na wale ambao watapata matatizo tumewaambia watoe ripoti kwenye balozi zetu ili hatua za kuwalinda na usalama wao kuwepo zichukuliwe. Kwa hiyo, hilo ndilo jibu.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Mji wa Tunduma ni mji unaokua kwa kasi na kuna miradi karibuni miwili au mitatu inatekelezwa kwenye Mji wa Tunduma, lakini tangu imeanza kutekelezwa mpaka sasa hivi wananchi hawajaanza kupata maji ya uhakika na Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri pamoja wamekuwa wakiwapa tarehe kila wakati za kumaliza miradi hiyo.

Je, ni lini miradi hiyo itakamilika ili wananchi wangu wa Mji wa Tunduma waanze kupata maji safi na salama kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza nashukuru kuona Mheshimiwa Mbunge anakiri kwamba tunafanya kazi kubwa na ipo miradi ambayo tunaitekeleza katika Jimbo lake. Kikubwa ambacho ninachotaka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama viongozi wa Wizara tumeshabainisha miradi ambayo ipo katika hatua mbalimbali kwa ajili ya ukamilishaji. Tumepanga katika wiki hii ya maji itakuwa siyo wiki ya mapambio, ni wiki kwa ajili ya kuzindua miradi yote ya maji, kwa hiyo Wakandarasi wajipange katika kuhakikisha wana-meet zile commitment tulizoziweka ili wiki hii ya maji tuweze kuzindua miradi mingi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunakualika katika kuzindua miradi yetu ya maji. Ahsante sana.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, Mji wa Tunduma ni sawa na Mji wa Mafinga na mji huu uko mpakani mwa Tanzania na Zambia na ni sura ya nchi ya Tanzania ambayo inapitiwa na Mataifa zaidi ya nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu wa uboreshaji wa miji hasa kwenye miundombinu ya barabara, unatakiwa ufanyike pia katika Mji wa Tunduma: Je, Serikali imejipanga namna gani kuhakikisha kwamba Mji wa Tunduma unapata barabara bora katika mpango huu ambao utaanza mwaka 2020.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru ndugu yangu kwa swali zuri la Tunduma. Nami nikiri wazi kwamba Tunduma ni miongoni mwa miji inayokua na hata katika kutembea kwetu pale, tulitembelea maeneo ya hospitali kuangalia miradi ya maendeleo, ni kweli kuna maeneo yana changamoto kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kama nilivyosema awal kwamba ni mpango wa Serikali, kwa sababu kuna ile miji ambayo ilianzishwa baada ya mpango kuanza, ambapo tulikuwa tumepata dola za Kimarekani karibu milioni 254, lakini pia kupitia mradi wa TSP tumetumia karibu milioni 840. Kwa hiyo, katika mpango wa sasa ni kwamba tutaweka Tunduma na maeneo yote yale ambayo mwanzo hayakuhusishwa katika ule mpango wa awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo kubwa ni kwamba, kama tulivyofanya katika miji yetu mikuu sasa hivi ukienda Mbeya, Tanga, Arusha, Dodoma, ukienda Babati, Iringa, Musoma, Tabora, kokote unakopita tumefanya uwekezaji mkubwa wa kujenga barabara za kisasa, kuimarisha miundombinu na tutaendelea katika hiyo miji mipya ambayo ipo Tunduma hapo baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na swali la msingi linalohusu Baraza la Kata, pia Mkoa wetu wa Songwe hauna Baraza la Ardhi la Wilaya. Nimekuwa nalalamika sana kwenye Bunge hili na Mheshimiwa Naibu Waziri alijibu kwamba jambo hili watalishughulikia haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi wananchi wangu wa Songwe wanakwenda Mbeya kusikiliza kesi zao na inasababisha gharama kubwa sana za kwenda kufika kule kusikiliza kesi na kurudi.

Je, ni lini Baraza la Kata litaanzishwa katika Mkoa wetu wa Songwe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa mujibu wa Sheria, tunatakiwa kuwa Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya kila Wilaya. Mpaka sasa Mabaraza yaliyoanzishwa kisheria yameshafikia 100, lakini yanayofanya kazi yako 54.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema kwamba tuko tayari kuanzisha Baraza katika Wilaya yoyote ili mradi pawepo na miundombinu ambayo itawezesha kuanzishwa kwa Baraza hilo. Kwa sababu kama Wizara, hatujengi majengo kwa ajili ya Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya. Kwa hiyo, kama wakiwa tayari; na nilipokuwa kule mwezi uliopita, waliitoa hoja hiyo, nikasema tunachohitaji ni kuonyeshwa eneo ambalo litatosheleza kuweza kuwa na Ofisi ya Baraza la Ardhi na Nyumba ya Wilaya. (Makofi)
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni lini Serikali itajenga barabara ya baypass ya kutoka Mpemba kwenda Tunduma kwa sababu ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati anafanya kampeni zake kipindi cha mwaka 2015?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakajoka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua umuhimu wa baypass na usanifu unafanyika, tutajenga mara moja tukipata fedha kwa ajili ya barabara hii.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kumekuwa na msongamano mkubwa sana kwenye magereza mbalimbali hapa nchini na hasa ukiangalia kwa mfano kama Gereza letu la Ilembo pale Vwawa wafungwa wanaotakiwa kukaa pale pamoja na mahabusu ni 120; lakini mpaka sasa hivi kuna mahabusu pamoja na wafungwa zaidi ya 400 na hili limekuwa ni tatizo katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua haya magereza kutokana na mrundikano huo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kumekuwa na matatizo makubwa sana katika magereza haya, hakuna zahanati katika magereza yetu na kumekuw ana tatizo kubwa sana la wafungwa kutolewa kwenye haya magereza na kupelekwa kwenda kutibiwa katika hospitali mbalimbali hapa nchini wakati huo magereza hawana magari.

Serikali ina mpango gani wa kujenga zahanti katika magereza yetu yote hapa nchini ili wafungwa na mahabusu katika maeneo haya wawe wanatibiwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna utaratibu wa kujenga magereza mapya, kuongeza mabweni na kupanua kadri ya hali ya fedha inavyoruhusu. Kwa mfano, katika kipindi cha karibuni tumekamilisha ujenzi wa Gereza la Ruangwa, Gereza la Chato lakini pia na kufanya uongezaji wa mabweni katika magareza kadhaa nchini, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba pale ambapo hali itaruhusu na Gereza la Vwawa vilevile nalo tutafanya upanuzi wa gereza hilo ingawa upanuzi wa magereza siyo njia pekee ya kupunguza msongamano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtakumbuka hivi karibuni, nichukue fursa hii kwanza kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kutokana na dhamira yake ya dhati ya kuwatumikia wananchi wa nchi hii hususani wanyonge na hasa pale katika jitihada zake za kuona kwamba wanyonge wa nchi hii hawaonewi, alivyofanya ziara katika Gereza la Butimba hivi karibuni alitoa maelekezo nchi nzima ambayo yameshaanzakufanyiwakazi na yamesaidia sana kupunguza idadi ya mahabusu ambayo kimsingi msongamano huu kwa kiwango kikubwa unasababisha na mahabusu ambao ni wengi wakati mwingine wanapita hata idadi ya wafungwa.

Kwa hiyo, baada ya maelekezo yale na hatua ambazo mbalimbali zimechukuliwa sasa idadi ya mahabusu imeendelea kupungua nchini na hivyo kupunguza msongamano.

Lakini kwenye eneo hili la pili la zahanati, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna utaratibu katika magereza yetu yote kuwa na madakrati pamoja na zahanati. Kwa hiyo, ninachoweza kusema ni kwamba katika maeneo ambayo tunaona labda kuna upungufu wa nguvukazi ya madaktari pamoja na madawa tufanye jitihada za kuongeza ili tuweze kukabiliana na changamoto ya wafungwa wetu na mahabusu ambao wanahitaji matibabu katika magereza. Kwa hiyo, hii kama katika Gereza la Vwawa ni changamoto nitalichukua na nifuatilie ni la ukubwa kiasi gani na tuweze kuchukua hatua stahiki.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza swali la nyongeza, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nakumbuka mwaka 2017/2018 Serikali ilitenga karibuni bilioni 900 kwa ajili ya shughuli za maendeleo kwenye Wizara ya fedha, na fedha hizi, zilikuwa zinakwenda kutoa elimu kwa walipa kodi watanzania, na sasa hivi kumekuwa na kero kubwa sana ya kodi kwenye nchi hii, na biashara nyingi zinafungwa katika Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, Je, Serikali imejipanga namna gani, namna ya kutoa elimu kwa walipa kodi ili Watanzania hawa waweze kujua wanalipa kodi kutoka kwenye faida, au wanalipa kodi kutoka kwenye mtaji? Kwa sababu elimu hiyo hawana mpaka sasa hivi, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwenye jibu langu la msingi, nimeelezea Elimu ya Kodi hutolewa katika ngazi mbalimbali, kuanzia ngazi ya Taifa Mamlaka ya Mapato Tanzania hukaa na Wafanyabiashara kuwapa Elimu ya Kikodi physically yaani uso kwa uso lakini pia kupitia Vyombo mbalimbali vya Habari.

Mheshimiwa Spika, lakini pia hata sisi Viongozi Wakuu wa Wizara ya Fedha tumekuwa tukizunguka katika Mikoa mbalimbali kukutana na wafanyabiashara na kupeana Elimu ya Kikodi tukiwa na Wataalamu wetu wa Kikodi. Lakini pia kila mwezi Wakuu wa Mikoa huwa na Mabaraza ya Biashara kwenye Mikoa yao, hukutana na wafanyabiasha na kutoa Elimu ya Kikodi Wataalamu wetu wa Kikodi wanakuwepo.

Vilevile Wakuu wa Wilaya wana Mabaraza ya Biashara ya Wilaya ambapo hukutana na wafanyabiashara, wataalam wetu wa Kodi wakiwepo na Elimu ya Kikodi hutolewa.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito kwa Watanzania, kwa Wafanyabiashara wote kuchukua jukumu la kuhudhuria Mikutano hii ili waweze kupata Elimu ya Kikodi na kero zao mbalimbali za Kikodi ziweze kutatuliwa.

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Mwakajoka amesema biashara nyingi zimefungwa, hili ni suala ambalo linaongelewa katika ujumla wake, nilishaliambia Bunge lako Tukufu kufungwa na kufunguliwa kwa Biashara ni jambo la kawaida katika Mataifa yote Duniani, siyo kwa Tanzania peke yake, na nilishaeleza, rate ya Biashara kufungwa ni ndogo kuliko rate ya Biashara zinazofunguliwa, nashukuru sana.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika Tunduma ni mpakani na kuna msongamano mkubwa sana wa malori yanayovuka mpaka wa Tunduma kuelekea Zambia, lakini pia wananchi wamekuwa wakipata shida sana ya kuweza kutumia barabara moja ambayo iko kwenye mji wetu wa Tunduma, lakini kuna bypass ya barabara inayotokea Mpemba kuelekea Tunduma Mjini kilometa 12 na Mheshimiwa Naibu Waziri alipita kuja kuingalia barabara ile na akatuahidi kwamba barabara ile ingeweza kujengwa katika mwaka huu wa fedha.

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ile ili kupunguza msongamano na kuwapa unafuu Wananchi wa kuendelea kutumia barabara yetu ya Mji wa Tunduma? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mji wa Tunduma unakua kwa kasi na ni ukweli inahitajika maboresho mbalimbali ya miundombinu katika eneo hili na Serikali inachukua hatua nyingi kupaboresha sehemu hii ya Tunduma kwa sababu hata ukifika pale utaona magari ni mengi sana na sisi tumejipanga pia kuboresha kwenye kituo chetu hiko cha Mpemba pale, tukatakuwa na ujenzi wa kituo kile ambacho kitashughulikia mambo mengi, Mheshimiwa Mwakajoka anafahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa Mwakajoka hapo amechomekea kidogo kusema nilitoa ahadi ya kujenga kiwango cha lami katika mwaka huu wa fedha, siyo kweli. Nilichokisema ni kwamba Serikali inayo mpango wa kufanya maboresho maeneo haya ikiwepo kuangalia zoezi zima la ujenzi wa bypass ili kukwepesha adha ambayo watumiaji wa barabara wanaipata wakipita katika Mji wa Tunduma hususan wanaokwenda maeneo ya Rukwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa kweli tulifanya mazungumzo na mimi pia niliwatahadharisha uongozi uliopo pale ili tuanze kuangalia mipango kwa mapana, kwa sababu mji ule unakua sana. Utaona ile hifadhi ya magari (parking) muda siyo mrefu zitafika mpaka kwenye Mji wa Mbozi, kwa hiyo, ukuaji ni mkubwa sana. Kwa hiyo, kwa upande wa Serikali sisi tunaona kwamba mipango yetu lazima tuiweke vizuri ili siku za usoni kulingana na ule ukuaji wa mji huu kwamba huduma zile muhimu zinapatikana.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Mwakajoka nakuomba uvute subira tu, wewe unafahamu umejaribu kuchomeka hapa lakini unafahamu kwamba umuhimu wa hii bypass lakini na sisi tumeichukua hiyo tunaendelea kuiweka kwenye mipango yetu ili kwa haraka tuje tuweke huduma hii ya barabara kwa maana ya bypass. Wewe vuta subira tu na ikikupendeza ukipata muda uje tuzungumze tuone kwenye strategic plan yetu tumeiweka namna gani ili hata ukipeleka information kwa wananchi wetu usiwaambie kwamba tutaanza kujenga mara moja, lakini uwaambie kutokana na hali ambayo ipo, kwenye utaratibu wetu ambao tumejiwekea ambao ni mzuri tu, kwa kweli tumewajali sana wananchi wa Tunduma.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA:Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Pamoja na majibu ya Serikali ya kuonesha masoko mbalimbali nje ya nchi, lakini ukweli tu ni kwamba Serikali hii imekuwa ikizuia sana wafanyabiashara wanaopata masoko nje kwa kisingizio kwamba kuna njaa na haijawahi hata siku moja kuweka mpango wa kufidia hasara ambazo zinatokana na zuio hilo la Serikali.

Sasa Je, Serikali imejiandaa namna gani kuhakikisha kwamba inawapa taarifa wakulima hawa na wafanyabiashara kwamba haya masoko yapo kwasbaabu Bunge sasa hivi haliko live?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili; Mheshimiwa Waziri amesema kwamba kuna mpango wa stakabadhi ghalani lakini katika mazao haya ambayo ni ya mpunga pamoja na mahindi hasa katika Nyanda za Juu Kusini mpango huu haujaanza kufanyakazi. Serikali ina mpango gani wa kuweka utaratibu huu wa stakabadhi ghalani katika mazoa ya mahindi na mpunga kwenye Nyanda za Juu Kusini?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kimsingi ufanyaji wa biashara katika nchi yoyote ile ni lazima uende sambamba na kuzingatia mahitaji halisi ya wananchi wake kwa faida ya wananchi wake. Lakini niseme tu kwamba kwa hali iliopo sasa tunacho chakula cha kutosha na nipende kuwajulisha Watanzania wote na wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi kwamba fursa ya kuuza mazao hayo nje ipo na pale ambapo mfanyabiashara atakwama basi aweze kuwasiliana na sisi kupitia simu zetu, kupitia mitandao ya Wizara ya Viwanda na Biashara, lakini pia Wizara ya Kilimo ambayo tunashirikiana ili kuondoa vikwazo ambavyo vinaweza kuwa vinamzuia mfanyabiashara kufanya shughuli zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili kuhusu Stakabadhi Ghalani; kimsingi ni kwmaba mfumo huo umeshaanza. Nimeshawahi kutembelea baadhi ya maeneo, kwa mfano, pale Tunduru tayari mfumo unatumika kwa masoko ya mpunga, soya pale Namtumbo na maeneo mengine, kwa hiyo niseme tu kwamba huu mfumo ni mzuri kwa sababu unamuwezesha mkulima kwanza kupeleka mazao yao kwa pamoja sehemu moja na kupata soko la uhakika lakini vilevile kuzingatia ubora unaohitajika.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba vijiji vitano mpaka sasa hivi vimeshakamilika kupata maji katika Jimbo la Momba ambapo jumla ya vijiji vilivyopata maji sasa hivi vitakuwa ni saba (7) lakini jimbo hili lina vijiji 82 ina maana kati ya vijiji 82 ni vijiji saba (7) tu ndiyo vyenye maji ya bomba. Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba katika bajeti hii ambayo imetengwa ya shilingi bilioni 1.7 inapelekwa kama ambavyo imetengwa ili kwenda kupunguza tatizo la maji kwenye Jimbo la Momba?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, mwaka 1973 katika Mji wa Tunduma uliazishwa mradi wa maji wa mserereko katika Kata za Mpemba na Katete. Mradi ule sasa hivi umekuwa ukitoa maji kidogo sana kutokana na kutokukarabatiwa kwa muda mrefu. Serikali ina mpango gani kukarabati mradi ule ili uwahudumie wananchi wa kata hizo mbili?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kutumia fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri. Kikubwa ambacho nataka kusema ni kwamba Ilani ya Chama cha Mapinduzi inatutaka itakapofika 2020 tuwe na 85% ya upatikanaji wa maji vijiji na 95% upatikanaji wa maji mijini.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo, sisi kama Wizara ya Maji tukaona chanzo pekee ambacho kinaweza kutatua tatizo la maji katika Mji wa Momba ni kutumia Mto Momba. Sasa hivi tupo kwenye hatua ya usanifu, mradi ule utakapoanza utaweza kuhudumia zaidi ya vijiji 21. Kwa hiyo, tunamhakikishia Mheshimiwa Mbunge tutafanya usanifu ule kwa haraka kwa ajili ya utekelezaji wa mradi mkubwa wa kuchukua maji Mto Momba na kuweza kuhudumia vijiji 21.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mradi wa ukarabati wa mradi wa maji kwa ajili ya kuhudumia Kata ya Mpemba, sisi kama Wizara ya Maji tutaongea na Wahandisi wetu Maji pale Tunduma kuhakikisha wanafanya ukarabati huo ili wananchi waweze kupata huduma hii maji. Maji ni uhai, sisi kama viongozi wa Wizara hatupo tayari kupoteza uhai wa wana Tunduma.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini bado kuna malalamiko makubwa sana kwa Madereva wa malori na mabasi na karibu asilimia 90 ya Madereva hao hawana mikataba ya kazi na kwa sababu Serikali inasema kwamba Mikataba yao ilitakiwa iboreshwe toka mwaka 2015 na mpaka sasa mikataba yao bado haijaboreshwa na bado hawajapewa mikataba.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuharakisha jambo hili ili wafanyakazi hao waweze kufanya kazi yao vizuri kwa sababu wakiwa na mawazo sana wanaweza wakasababisha ajali na Watanzania wengi wakapoteza maisha?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kumekuwa na tatizo kubwa sana kwa sisi ambao tunaishi mipakani na mmeona kuna migomo mingi sana inatokea pale Tunduma watu Madereva wanapaki malori kwa sababu tu ya migongano kati ya wamiliki wa mabasi na malori kwa ajili ya mikataba hiyo? Sasa Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba jambo hili linakwisha haraka kwa sababu ni muda mrefu sasa na Serikali ipo, inatoa majibu humu Bungeni lakini utekelezaji unakuwa hakuna? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Frank Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, maswali yake nitayajibu yote kwa mkupuo. Katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 na katika ahadi ambayo Mheshimiwa Rais aliitoa akiwa Kahama mwaka 2015 juu ya Mikataba ya Wafanyakazi na hasa Madereva, Serikali inakuja na mpango mkakati ufuatao, hatua ya kwanza ilikuwa ni kuwataka Wamiliki wote wa Mabasi na Malori ambao watakwenda kuomba SUMATRA leseni ya usafirishaji wahakikishe kwamba wanawasilisha na Mikataba ya Wafanyakazi kama eneo la kwanza la kuhakikisha kwamba Madereva hawa wanapata mikataba yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza hili, Serikali tumekuja na mkakati tofauti tumeona kwamba mkakati huu ulikuwa una mianya ya utekelezaji wake hivyo, siku mbili hizi zijazo Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu na Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, watatoa tamko na maelekezo ya kuanzia tarehe moja mwezi Julai ni hatua gani zitachukuliwa. Kuanzia hapo nina hakika kwa mkakati huo ambao wameuweka ni kwamba kila Dereva wa nchi hii atakuwa na mkataba wake na tutahakikisha kwamba pia kila Mmiliki wa Chombo cha Usafiri anafuata masharti ya sheria kama Kifungu cha 14 cha Sheria za Ajira na Uhusiano Kazini kinavyosema. Kwa hiyo, nimwondoe tu hofu Mbunge kwamba si maneno tu lakini mkakati umeshawekwa vizuri kabisa na tumekaa na wenzetu wa Jeshi la Polisi muda siyo mrefu kuanzia tarehe Mosi, Julai mtaona cheche za Wizara.