Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Abdallah Dadi Chikota (1 total)

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu ni sera ya nchi yetu kuhakikisha kwamba bandari zetu zinapanuliwa na kuboreshwa na ili ziweze kuwavutia wafanyabiashara wa nchi jirani kutumia bandari zetu, na hii tumefanikiwa sana kwa Bandari ya Dar es Salaam.

Swali langu je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuhakikisha wafanyabiashara wa Sudan Kusini na Uganda wanaitumia Bandari ya Tanga na wafanyabiashara wa Congo, Malawi na Zambia wanaitumia Bandari ya Mtwara? Nakushukuru. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Bismillah.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chikota, Mbunge wa Nanyamba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali yetu kupitia Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imetenge fedha kwa ajili ya maboresho ya bandari zetu zote nchini, zile zilizoko Ukanda wa Bahari Kuu pia kwenye Maziwa Makuu ya kuimarisha miundombinu na huduma mbalimbali. Mkakati wa Serikali ambao Mheshimiwa Mbunge anataka kujua wa namna ya kuvutia matumizi ya bandari hizi kwa nchi jirani ipo na inasimamiwa pia na Wizara yetu ya Wizara ya Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Spika, moja tunaongeza vifaa vinavyoweza kupakua na kupakia mizigo kwa muda mfupi ili kuwahakikishia wale wateja wetu kuwa matumizi ya bandari yanatumika kwa muda mfupi zaidi, lakini mbili, tumefanya mapitio ya tozo hasa kwa Bandari ya Tanga na kule Mtwara tumetoa fursa ya kupunguza tozo ili kuvutia kulinganisha na mahitaji ya Dar es Salaam kwa sababu Dar es Salaam wingi wa meli ni mkubwa sana kuliko Bandari ya Tanga na Dar es Salaam ambako pia hata msimu uliopita tumekuwa tukilishughulikia hili na hatimaye tukafikia hatua ya kupunguza tozo ya asilimia 30 ya meli yoyote inayokwenda Tanga kwa ajili ya kuwezesha nchi kama Somalia na Sudan ili kuweza kutumia Bandari ya Tanga na kule Mtwara kwa nchi kama Malawi, Zambia na hiyo Congo ambako pia ni rahisi kufika ili wale wateja wanaoleta mizigo kwenye Bandari hizi za Mtwara na Tanga waweze kuvutiwa zaidi..

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili tunaamini sasa tunaweza tukawavutia wengi kwasababu wakija Dar es Salaam tozo ni kubwa na pale Mtwara na Tanga tozo ni ndogo. Lakini bado tunaangalia pia kwenye eneo la ushushaji wa mafuta nako tumeimarisha vituo na zile mita za kushushia mafuta. Kwa hiyo, tunakaribisha pia na meli zinazoshusha mafuta kwenye bandari zetu za Mtwara na Tanga; na tumejenga pia na matenki ya kutosha. Kwa hiyo urahisishaji wa kazi kwenye bandari hizo ni rahisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, lakini Mamlaka ya Bandari tumeona ikifanya jitihada mbalimbali kupitia Balozi zetu zilizoko kwenye nchi hizo kuhamasisha wafanyabiashara wa nchi hizo kutumia bandari zetu. Hili linaendelea na tumefungua pia hata ofisi za Mamlaka ya Bandari kama vile Congo na tumefungua ofisi Malawi, Zambia ili wateja wote wanaohitaji kupata huduma kupitia bandari yetu na bandari zetu zote watapata mawasiliano kwenye nchi zao bila ya kuwataka wao kuja Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na jitihada nyingine nyingi ambazo tunazifanya ikiwemo na elimu ya kuelimisha wafanyabiashara mbalimbali kutumia bandari zetu za Tanzania. Lakini wote mnajua kwamba Serikali ya Awamu ya Sita nayo inaendelea kusimamia ukamilishaji wa reli ya kati ambayo itakuwa inabeba mizigo; ukamilishaji wa barabara ambako pia magari makubwa yatapita yakiwa yamebeba mizigo haya yote tunaamini wanaelewa.

Mheshimiwa Spika, na nitoe wito kwa wafanyabiashara wa ndani ya nchi na nje ya nchi kutumia vyema bandari zetu zote zilizoko ukanda wa Pwani pia kwenye maziwa yetu tuweze kuruhusu kuongeza uchumi zaidi kwenye nchi yetu na kwa mataifa ya nje tuwahakikishie usalama. Tanzania ni nchi salama na tumeendelea kuimarisha usalama ndani ya nchi. Kwa hiyo tunawahakikishia usalama wa mizigo yao. Wao wenyewe wanapoingia lakini pia wanapopeleka mizigo kwenda kwenye nchi zao. Haya yote tunaamini wafanyabiashara kupitia forum pia za mikutano ya wafanyabiashara wa Tanzania na nchi hizo itaendelea pia kutoa elimu kwa nchi hizo kuleta mizigo na kutumia bandari yetu kuchukulia mizigo. Ahsante sana. (Makofi)