Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Jasmine Tiisekwa Bunga (14 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi katika Bunge lako hili Tukufu. Kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama na kuongea, nilikuwa naendelea ku-observe majadiliano yanavyokwenda.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu na kumpongeza sana Mheshimiwa wetu Rais kwa jinsi anavyopambana katika kuondoa umaskini, kupambana na rushwa, mafisadi na kadhalika ili kuona kwamba sasa nchi yetu itafikia mahali ambapo ile keki itagawanywa mpaka kule kwa wanyonge. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza mama yetu Mheshimiwa Samia kuwa mwanamke wa kwanza kuongoza Taifa hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kazi tunaiona, nawapongeza Mawaziri wote kazi zetu tunaziona na mnatosha lakini pia kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa kurudi mjengoni na wengine mara yetu ya kwanza kama hivi. Niwapongeze wapiga kura wangu wa Mkoa wa Morogoro pamoja na wanawake UWT Taifa kwa kuniamini kuweza kuwawakilisha bila kusahau support ninayoipata kutoka kwa familia yangu ikiongozwa na mume wangu mpendwa Profesa Tisekwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, napenda sasa niweze kuchangia hii bajeti. Nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na timu yake yote akiwemo Mheshimiwa mdogo wangu Dkt. Ashatu Kijaji, nafahamu uwajibikaji wake na weledi wake, kwa hiyo nawapongeza sana. Bajeti hii inaleta matumaini hasa kwa kutenga asilimia 40 kupeleka kwenye masuala ya miradi ya maendeleo, hongereni sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naungana na wajumbe wote ambao wamejadili suala hili hasa kwa kuwapongeza jinsi walivyopanga mikakati ya kuweza kukusanya kodi na kuongeza wigo wa kodi, nawapongeza sana. Pia nashauri sasa tuangalie zile kero ambazo zinaambatana na kodi na tozo za aina fulani ambazo wananchi bado wanazilalamikia kama Serikali muweze kuangalia kwa undani na kwa macho mawili ili kuondoa misuguano ambayo inaweza ikatokea kati ya Serikali na wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nichangie kwa kusema kwamba sasa hivi Watanzania sera yetu ya maendeleo tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda baadaye kufikia uchumi wa kati. Viwanda peke yake bila ya kuwa-empower wananchi wake hasa wananchi waishio vijijini haviwezi vikawa endelevu. Kwa nini nasema hivyo? Ni lazima tuweze ku-empower maendeleo vijijini na kwa wananchi wa vijijini kwa sababu asilimia 75 ya wananchi wako vijijini, rasilimali nyingi za Taifa zipo kijijini, nguvu kazi ipo vijijini lakini umaskini uliokithiri upo vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna sababu zote za msingi kuhakikisha miradi hii ya maendeleo ambayo imeelekezwa vijijini zile fedha ambazo zimepangwa basi fedha hizi zote zipelekwe ili kuendeleza vijiji vyetu. Tukifanya hivyo tunaweza sasa kuwa-empower hawa wananchi wetu na kuweza kuwa na purchasing power kwa sababu ukiwa na kiwanda parameter mojawapo lazima ku-create soko la ndani na la nje. Kama watu wako ni maskini ina maana hivi viwanda sustainability yake kidogo inaweza ikawa kwenye question mark. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuangalie suala la usawa wa kijinsia. Miradi ambayo imeelekezwa kule vijijini au mijini ile yote ambayo imelenga kupunguza matatizo ya wanawake (reproduction roles zao) mfano maji, afya, elimu na kadhalika ipewe fedha kama ilivyokuwa imepangwa. Kama tunavyoona 51% ya population ya Tanzania ni wanawake, ukiwaacha watumie saa tabi au sita kwenda kuchota maji, kuhangaika kwenda kwenye kituo cha afya hawataweza kushiriki katika uzalishaji. Kwa hiyo, huyu mwanamke ili aweze kuwa productive kwa sababu wako wengi na waweze kujikwamua kiuchumi tufikie ile fifty fifty mwaka 2030, lazima hawa wanawake wapunguziwe ile mizigo ya reproduction roles. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda nizungumzie suala la shilingi milioni 50. Hii shilingi milioni ya kila mtaa naona kwamba imeelekezwa sana kwa wajasiriamali na SACCOS. Mimi naona hii approach tunayoitumia siyo sahihi sana kwa sababu tunasahau hili kundi la maskini wa kipato cha chini watakuwa hawana msaada.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini Sh. 5,000 inaweza ika-transform maisha ya huyu maskini ambaye hana kitu. Kwa sababu kule kijijini huyu mtu maskini wa kipato cha chini ambao wanaishi under poverty line kwa mfano anaweza akawa na nguvu, yupo physically fit, ana ardhi lakini hana jembe, hana mbegu. Kwa hiyo, huyu mtu ukamkopesha Sh. 5,000 akanunua mbegu, akanunua jembe that means next season tayari umeshamwezesha lakini sasa tukijikita kwenye wajasiriamali tukawasahau hawa, hatutafika mbali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine nasema sasa ili kupunguza milolongo ya kodi na tozo kwa wananchi wetu tutumie rasilimali zetu kwa mfano utalii, madini na kadhalika. Sisi kule Morogoro (Kisaki) tuna hot spring eneo kubwa, kilometers and kilometers lakini halitumiwi. Kwa mfano, ukienda Swaziland walikuwa na ka-spot kamoja ka hot spring wamejenga pale hoteli, swimming pool, hela zinatengenezwa. Sisi kwetu ukienda kwenye zile hot spring unakuta vibanda vya waganga wa kienyeji vimejazana pale. Kwa hiyo, tutumie rasilimali zetu ili tuweze kupunguza hizi tozo ambazo mara nyingi ni kero kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Kitengo cha Monitoring and Evaluation lazima kipewe kipaumbele kwa sababu on desk work mtu anakuja anatengeneza mikakati bila research, tathmini, hatutafika mbali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie upande wa environment. Sikubaliani na kusema mifuko ya plastic sijui microns 50 sijui nini, nashauri ipigwe marufuku, inailetea hasara Taifa letu. Mafuriko haya mengi ukiangalia ni kwa sababu ya mifuko ya plastic. Huyu mzalishaji mwenye kiwanda anapata super profit lakini Serikali inapata super loss kwa sababu kila mwaka lazima itengeneze miundombinu ya barabara, umeme na kadhalika. Kwa hiyo, mimi naona hapana, ikatazwe kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho napenda nimalizie kwa kusema kwamba, mimi nashangaa sana, Waheshimiwa Wabunge, wachumi, wasomi na kadhalika kazi yao kusimama kwenye media na kubeza Serikali. Hii bajeti tunayoipitisha ni ya Serikali lakini kila Mtanzania lazima awe na bajeti yake ku-top up kwenye bajeti ya Serikali. Mimi nashangaa kwa mfano ukienda Bangladesh, Profesa Yunus alichukua dola zake 27 kwa kila mwanamke wale waliokuwa wanatengeneza furniture mpaka ikazaa Grameen Bank ambayo na yenyewe ikazaa na vingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii Profesa mzima aliyebobea anaenda eti kwenye media kuanza kulaumu Serikali, wewe Mbunge unasimama unalaumu Serikali eti mpaka nipewe nafasi ya kwenda Ikulu, wewe role yako ni nini kama Mbunge, kwa sababu wewe ni kiongozi! Wewe role yako ni nini kama Profesa kwa sababu wewe ni kiongozi, wewe role yako ni nini kama mwananchi wa kawaida kwa sababu sasa hivi mpaka Mheshimiwa Rais aende akawafanyie watu usafi kwenye kaya zao, inakuja hiyo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nasema bajeti ya Serikali lazima iwe supported na sisi wananchi kwa umoja wetu. Watu hapa ni mabilionea badala ya kuweka hela benki chukueni hizo pesa wagawieni kama alivyofanya huyu Profesa Yunus wa Bangladesh kwa riba nafuu. Kwa sababu bajeti ya Serikali hata siku moja haiwezi kutosheleza kuleta maendeleo ya nchi yetu, ni sisi. Vita dhidi ya umaskini ni vita na kila mwananchi lazima awe askari. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nasema, naomba bajeti hii fedha zipatikane ili kuweza kuleta maendeleo. Naunga mkono hoja, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Mapendekezo ya Mpango huu unaoendelea. Kwanza kabisa, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na timu yake yote kwa kutuletea huu mpango mapema zaidi ili tuweze kuufanyia kazi, uboreshwe na baadaye tuweze ku-achieve yale ambayo tunatarajia kuyafanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumpongeza sana Mheshimiwa wetu Rais wa Awamu hii ya Tano kwa nia njema kabisa ya kutaka kuleta maendeleo ya nchi hii hasa ukiangalia kwamba anataka keki ya Taifa igawanywe kuanzia kwa mwenye kipato cha chini mpaka mwenye kipato cha juu. Kwa hiyo, jitihada nyingi sana anazifanya na tukizingatia kwamba yeye ndiyo mara yake ya kwanza kushika uongozi ni lazima kutatokea changamoto za hapa na pale. Kwa mfano, anapambana na ufisadi, rushwa, wafanyakazi hewa, matumizi mabaya ya Serikali na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotokea sasa hivi kwa mtazamo wangu, watu wanalaumu wanaona kwamba it is a government failure, kwangu mimi sioni kwamba Serikali imeshindwa, ni muda mchache, hapa tupo kwenye transitional period, kwamba kuna reforms nyingi zinafanyika ili tuweze ku-achieve haya ambayo Mheshimiwa Rais wetu anayataka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika change ya aina yoyote huwa kuna early adapters, slow adapters na late adapters kwamba wapo wale wanaokubali mabadiliko haraka sana na wapo ambao tayari wanampongeza Mheshimiwa Rais, hawa ni wale wanyonge ambao haki zao hazitolewi. Hata hivyo, wapo wale ambao wanakubali taratibu tunawaita slow adapters, hawa wanaangalia kwanza mazingira wajiweke sawa, lakini kuna wale late ambapo yeye anasubiri kwanza mambo yafanikiwe ndiyo aende.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kinachotokea kutokana na change, wale wanaolaumu inawezekana ni katika kundi la wale watu ambao ni mafisadi, wala rushwa ndio wanamkwamisha Mheshimiwa Rais wetu. Kwa hiyo, hawa kwa vyovyote hawawezi kukubali hizi reforms ambazo zimepangwa ili tuweze ku-achieve kwamba sasa keki ya Taifa wafaidi wananchi kuanzia wa kipato cha chini mpaka kipato cha juu. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi anayoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni kwamba sasa tumpe support kwa sababu kila utawala mpya lazima utakuwa na changamoto zake. Yeye ni mara yake ya kwanza. Tukianza hata kihistoria Mwalimu Nyerere wakati amepokea utawala kutoka kwa wakoloni alipambana sana kwenye ujamaa na wapo watu ambao walikuwa ving’ang’anizi ndiyo wakatuletea hata huu ujinga ujinga wa structural adjustment ambayo hailingani. Kwa hiyo, alipambana na watu wengine walikataa kwa sababu ya maslahi yao, tuliwaona kina Kambona walikimbilia nje, ndiyo hiyo hiyo ambayo inatokea sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija upande wa Mheshimiwa Mstaafu Rais Mwinyi, watu walimuita ruksa lakini kutokana na mazingira aliyoyakuta wakati ule, bidhaa hamna akafungulia. Kwa hiyo, ni kama vile tunavyosema kila zama na kitabu chake. Pia ukiangalia wakati wa Mheshimiwa Mkapa watu waliita ukata lakini mwaka wa kwanza aliyumba baadaye mambo yakaenda, vizuri sasa hivi tunamkumbuka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija upande huu wa Mheshimiwa Rais wetu aliyestaafu juzi, Rais Kikwete, wengi wakasema labda mpole lakini alifanya mambo makubwa lakini mwanzoni alivyoanza watu wakaona haendi. Sasa na hii Awamu ya Tano, hizi reforms jamani nani anayetaka ufisadi uendelee au rushwa iendelee, wafanyakazi hewa, tunapoteza fedha bure, ndiyo hiki kinachofanyika. Kwa hiyo, tumpe support Mheshimiwa Rais wetu afanye kazi na sisi Watanzania ndiyo tunaotakiwa tumuunge mkono badala ya kumbeza na kuibeza Serikali. Nafikiri hii siyo vizuri kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande sasa wa mpango, naomba nichangie kuhusu viwanda. Sera ya viwanda ni nzuri lakini tuangalie, je, Tanzania sasa hivi tunataka viwanda vya aina ngani? Kwa sababu sasa hivi tukumbuke tuko kwenye utandawazi, ni free market, tusije tukatengeneza kiwanda ambacho tunategemea labda soko la ndani tuko karibu milioni 50 labda consumers ni milioni 20, kwa hiyo soko la ndani halitoshelezi. Tufanye utafiti na soko la nje, siyo kwamba viwanda ili mradi viwanda. Nia ya viwanda ni kuajiri watu wengi mbali ya production, kwa hiyo, tuhakikishe tunaanzisha viwanda vile ambavyo vitawalenga hawa watu wetu wa chini waweze kupata ajira hasa vijana wetu wanaomaliza vyuo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna hili suala la kodi na tozo nyingi. Niungane na wenzangu, jamani sasa wasi-take advantage ya Serikali kukusanya kodi, kufanya mauzauza huko kuiharibia Serikali na ndiyo kinachofanyika sasa hivi. Kwa hiyo, tunaomba sana Waziri aliangalie suala hili, zile kodi na tozo ambazo ni kero kwa wananchi ziondolewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ukienda kwenye mabenki kwa mfano CRDB, jamani ukitaka statement ya karatasi moja ni Sh.11,000/= hivi kweli! Ile si ni ku-print out tu kwa nini wasitoze hela kidogo lakini sasa watu wanatengeneza business. Sasa hivi ukitumia ile mashine ya CRDB labda umeenda kununua kitu wanakata asilimia tano ya value ya kile kitu ulichonunua. Kama ni shilingi milioni tatu asilimia tano ya milioni tatu inakatwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni wizi kwa sababu wewe ni mteja wao lazima wakupe hizo fursa, wachukue hata elfu moja kama vile unavyochukua kwenye ATM, kwa hiyo hizi ni kero. Hata parking fee hizi za magari jamani kwa siku mtu akipaki Sh.1,000x30 ni Sh. 30,000, Sh. 30,000x12 ni Sh. 360,000 hiyo ni mbali na tax nyingine ambazo tunalipa. Kwa hiyo, kodi kama hizi ziangaliwe either zitolewe au zipunguzwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ni emphasize kwenye maendeleo vijijini, hii ni area yangu maendeleo vijijini. Huwezi ukawa na uchumi wa kati bila ya kuwa-empower hawa watu wa vijijini. Kwa hiyo, naomba miradi ya maendeleo ile iliyoachwa 2014/2015, 2015/2016 ipewe kipaumbele ili ile continuity ya kuleta maendeleo na ile Tanzanian vision iweze kuwa achieved. Tukiiruka ile tukaanza na hii mipya hatutaweza kufika kule, programu zetu zitakwama. Kwa hiyo, ni-emphasis tuangalie vitu ambavyo ni mahitaji ya msingi vijijini kama vile maji, elimu, barabara na masoko kwa ajili ya mazao yao. Tuki-promote hivi naamini kabisa huu uchumi wa viwanda na kipato cha kati utafanikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia kitu kingine, tusi-undermine human capital, ili tuweze kupata maendeleo lazima tuwekeze kwenye capacity building. Kwa hiyo, hizi semina za ndani na nje ni lazima hawa washiriki kwa sababu kwa dunia hii ya utandawazi ya sasa hivi kuna new technologies, new skills, new approaches concept ili tuweze kuingia kwenye hili soko la dunia na sisi tuweze ku-compete. Otherwise tukiangalia tu miradi tukasahau kwenye human capital itakuwa ni shida sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kweli naipongeza Serikali, napongeza Mapendekezo ya huu Mpango ambao umeletwa ili tuyafanyie kazi, tuboreshe badala ya kubeza na kudharau, hapana, huu ni mwanzo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha azingatie haya maoni ambayo wachangiaji mbalimbali wanatoa, yale ambayo tunaona kweli yanafaa ili kuboresha huu mpango na hatimaye nchi yetu iweze kufikia maendeleo endelevu ifikapo 2030.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii. Pamoja na kwamba dakika ni tano lakini mimi kama Mjumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii sitaacha kuipongeza Serikali yangu pamoja na Mheshimiwa Waziri kwa juhudi kubwa walizozifanya kwa muda mfupi katika kuboresha huduma ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli tumejionea, ukiangalia pale Ocean Road akina mama wengi wanafariki kwa sababu ya cancer lakini kumeboreshwa kwa hali ya juu. Sasa hivi kusubiri mionzi sio miezi mitatu ni wiki sita na tunaelekea wiki mbili, huduma ya dawa kutoka asilimia nne mpaka asilimia 60 bado vifaa vya kupima pamoja na PET Scan ambayo itapunguzia gharama Serikali lakini pia kuokoa maisha ya Watanzania hususan wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri atusaidie Mkoa wetu wa Morogoro, ni mkubwa sana tuna Wilaya nane, lakini Hospitali za Wilaya ni chache sana. Kwa hiyo, ili kupunguza vifo vya akina mama inabidi kwa kweli uliangalie suala hili ingawa kwako inakupa shida sasa inabidi uende TAMISEMI ndiyo maana tulisema kama inawezekana Waziri wa Afya ashuke mpaka chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nijikite kwenye Idara ya Maendeleo ya Jamii. Idara hii inachukuliwa kama kitu ambacho hakina umuhimu na mpaka kuna viongozi wa kitaifa wakisimama wanasema hawa walioajiriwa hawaoni kazi yao, lakini wanasahau kwamba Idara ya Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii ndio engine ya maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

Sasa hivi Tanzania wananchi hawaelewi, hamna mtu wa kuwaunganisha wananchi na Serikali yao, utakuta wanaunganishwa na wanaharakati. Mwanaharakati hata siku moja haisaidii Serikali, kazi yake ni kukosoa lakini hawa Community Development Officer na Social Workers ndio kiini na ndio hasa engine ya maendeleo. Kwa hiyo, tunaomba hii fedha sasa iliyotolewa itolewe yote muende kufufua sekta hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, watu wanafikiri kwamba uchumi unaletwa na wanauchumi na sayansi asilia, siyo kweli. Baada ya industrial revolution watu walipata social problem nyingi, wana-commit suicide, wanatumia dawa za kulevya, family breakdown, watoto wa mitaani, maadili, sisi tunabaki kupiga makelele lakini kazi kubwa ni hii ya Idara ya Maendeleo ya Jamii. Tukiweza kuiboresha wao ndio wanaotafuta solutions kwamba wafanye nini katika jamii yao. Utakuta sasa hivi hata barabara ikiharibika wanasubiri Serikali, kujenga vyoo wanasubiri Serikali kwa sababu hakuna mtu wa kuwaongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, sana Idara hii ya Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii ipewe kipaumbele. Ikiwezekana sasa tuboreshe vyuo vyetu kama cha Tengeru, kule kumechakaa, hakuna training, watu hawana new skills, tunategemea maendeleo yatatoka wapi? Tusione kwamba maendeleo ni kitu kingine hapana, tuanzie hapa chini. Kwa hiyo, naomba sana Serikali yangu Tukufu iweze kuangalia suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba sasa niongelee suala la UKIMWI. Wale watu wanaoishi na VVU tunaomba halmashauri iwasaidie wapate CHF ili waweze kupata septrin wanaumia sana kule, hakuna dawa na vitu vingine. Kwa hiyo, ombi lao kubwa dawa hizi za septrin ziweze kupatikana ingawa ni sehemu ya Halmashauri, lakini sasa ndiyo bado tunarudi kwenye changamoto ileile kwamba Wizara ya Afya kama itaishia kwenye sera haiwezi kuangalia utekelezaji wa sera zake mpaka huku chini bado tutaendelea kupata matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MASUALA YA UKIMWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa tena nafasi ili niweze kuhitimisha hoja hii ya Kamati. Kwanza napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wameweza kuchangia hoja yetu ya Kamati na tulikuwa na wachagiaji jumla ya 11.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ambao wamechangia kwa maandishi walikuwa ni watano na waliochangia kwa kuzungumza walikuwa sita. Kwa sababu ya uchache wao napenda kuwatambua ambao walikuwa ni Mheshimiwa Silafu Maufi, Mheshimiwa Lucia Mlowe, Mheshimiwa Mary Muro, Mheshimiwa Rhoda Kunchela na Mheshimiwa Jaqueline Ngonyani Msongozi hawa wamechangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wapo sita ambao wamechangia kwa kuzungumza ambao ni Mheshimiwa Lubeleje, Mheshimiwa Mwalongo, Mheshimiwa Mtolea, Mheshimiwa Mushashu amepongeza, Mheshimiwa Nuru Bafadhili na Mheshimiwa Bura naye amepongeza. Kwa hiyo, tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu ambayo kwa kweli michango hii ni mizuri sana na ina tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nawashukuru na Wabunge wote ambao hamkuchangia kwa sababu inaonesha kwamba mmekubaliana na taarifa na mapendekezo na maoni ya Kamati na ninyi pia tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Mawaziri wamechangia Waheshimiwa Naibu Mawaziri wawili, Mheshimiwa Naibu Waziri Stella Alex Ikupa pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri Antony Peter Mavunde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Wabunge hoja nyingi ambazo wamezichangia ni hoja ambazo kwa kweli Kamati iliziona na ilizitolea ushauri na mapendekezo. Kwa hiyo haja zote ambazo zimetolewa hakuna hoja ambayo imepingana na maoni na ushauri wa Kamati katika kuishauri Serikali ili iweze kuboresha huduma hii ya masuala ya UKIMWI na masuala ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, issues kubwa ambazo zilikuwa zimejitokeza wengi wamepongeza, lakini pia wamezungumzia upande wa ajira kwa vijana ambayo Kamati pia imeona ili kuweza kuwapatia activities ambazo zinaweza zikawapa kipato ili wasijiingize kwenye masuala ya UKIMWI na masuala ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia masuala ya lishe ili iweze kupata virutubisho, fedha za UKIMWI kwamba ziwanufaishe wale waathirika siyo kwa ajili ya semina. Issue nyingine iliyoongelewa ni umbali wa vituo vya kutoa dawa za ARVs ambazo pia Kamati tumeiona, lakini kwa sasa hivi tunaipongeza Serikali kwamba vipo vituo zaidi ya 6,000 tukiangalia huku mwanzo ambapo tulianza na vituo 20 na baadaye tukazidi kuboresha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la ushoga na usagaji na lenyewe limezungumzwa kama vinaongeza matatizo ya maambukizo ya UKIMWI. Pia na madawa ya kulevya na Kamati pia imeliona hilo na tumeshauri Serikali katika kuweza kuwa-empower hawa vijana ili waweze kujitambua na kufanya shughuli halali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dawati la kijinsia imependekezwa kwamba zile kesi ziende haraka, pia Kamati iliona na tumeshauri Serikali kusimamia vizuri hili dawati, bajeti ndogo pia hata Kamati imezungumzia. Sera ya UKIMWI kwamba imepitwa na wakati na yenyewe Kamati imezungumzia imetoa ushauri kwamba sasa irekebishwe na kuweka program mashuleni pamoja na ndoa za utotoni

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hii ni michango ya jumla ambayo Waheshimiwa hawa Wajumbe 11 wameweza kuchangia kwa maandishi au kwa mazungumzo. Kwa hiyo hoja zao zote kwa kweli ukiangalia ni hoja za msingi kwa sababu hazitofautiani na ushauri na mapendekezo ya Kamati. Tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge ambao mmeweza kusisitiza umuhimu wa kuweza kuboresha areas hizi ambazo nimezitaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani za pekee sasa nizipeleke kwa upande wa Serikali ambapo Waheshimiwa Naibu Waziri Stella Ikupa pamoja na Naibu Waziri Mavunde wameweza kutoa michango yao. Kwa upande wa Mheshimiwa Naibu Waziri Ikupa yeye alijikita kwa upande wa UKIMWI, kwa hiyo utakuta mambo aliyoyazungumzia tunashukuru kwamba mmeweza kuchukua ushauri na mapendekezo ya Kamati, tunawashukuru sana, kwa sababu Kamati ilikuwa imesisitiza kwamba UKIMWI upo na kila mtu anatakiwa awe balozi kujilinda yeye na kumlinda mwingine, tunashukuru kwa Serikali kuliona hili naamini kwa njia hii fedha zitatengwa ili kutoa elimu zaidi na watu waweze kujitambua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Naibu Waziri Ikupa alizungumza kuhusu suala la sera kupitwa na wakati, amelitolea ufafanuzi tunashukuru sana kwamba mchakato unaendelea. Vyanzo vya uhakika vya Mfuko wa AIDS Trust Fund Serikali imelipokea kwa sababu sasa hivi kwa upande wa UKIMWI tunategemea asilimia 90 fedha za wafadhili, wanatumia karibu bilioni 200 kwa mwaka kununua dawa za ARV.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku wakikata ule uzi, nafikiri mnajua shughuli itakavyokuwa. Kwa hiyo, ni vizuri sasa Serikali kuanza kujiandaa mapema kuwa na chanzo cha uhakika kama tulivyosema kule kwenye Mfuko wa REA au Mfuko wa Barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali inaendelea kuchangia kweli tumeona zaidi ya bilioni moja na zaidi zimetolewa, tunapongeza sana Serikali kwa upande huu wa Mfuko wa UKIMWI, kuna wakati kulikuwa na malalamishi mengi kwa ajili ya ukosefu wa dawa hizi za septrine kwa ajili ya magonjwa nyemelezi. Hata hivyo, tunashukuru sana tulimweleza Mheshimiwa Waziri Jenista akaipokea hoja yetu Serikali imetoa milioni 600 kuweza kununua hizi dawa, tunapongeza sana Serikali kwa kuweza kupokea ushauri wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la Njombe limezungumzwa Serikali imetoa ufafanuzi kwamba kulingana na survey iliyofanywa mwaka huu ilizinduliwa juzi tarehe Mosi Desemba kwamba ni kweli Njombe bado kuna tatizo. Kwa hiyo, tunapenda sana wenzetu wa Njombe kuweza kuendelea kutumia afua mbalimbali ili kuweza kupunguza UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri Antony Mavunde alijikita kwa upande wa madawa ya kulevya. Naye amekiri kwamba bajeti ni ndogo, ambayo Kamati pia imeona kwamba bajeti ni ndogo. Pia amekiri kwamba Sera ya Taifa ya Dawa za Kulevya inatakiwa haraka sana na ametuhaidi kwamba mchakato unaendelea. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuweza kuongea na Waziri wa TAMISEMI kwamba sasa zile Kamati za UKIMWI kwenye Halmashauri ziweze kuingiza dawa za kutibu waathirika wa dawa za kulevya ni vizuri sana kwa sababu kule ndiko kwenye watu. Tunashukuru pia Serikali kusema itaendelea na mkakati wa kuongeza vituo vya methadone katika Mikoa hiyo mitano ya Arusha, Kilimanjaro, Pwani, Morogoro na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru na hii ya Dodoma kwa sababu tayari ipo tayari na Mwanza basi kama mtafanya haraka tutashukuru sana itasaidia kwa sababu waraibu wa dawa za kulevya ni wengi mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia limezungumziwa suala la unyanyapaa kwa waraibu wa dawa za kulevya. Tunashukuru Serikali kwamba sasa Dodoma kituo hiki kitamalizika ili kuweza kutoa elimu ya ufundi. Kwa sababu changamoto kubwa wale waraibu wakishapata ile tiba wakawa vizuri, wakiwa idle hawana kitu cha kufanya, watarudia tena kule walikotoka. Kwa hiyo, tunashukuru sana Serikali kwa kuweza kufikiria kutoa elimu hii, lakini pia kuhakikisha kwamba kila Mkoa kutakuwa na dirisha maalum kwa ajili ya kutolea dawa hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawapongeza sana kwa kuongeza ile ceiling ya dawa kutoka kilo 120 hadi 300. Kwa kweli tunawashukuru sana sana kwa hii inaonesha kabisa nia ya dhati ya Serikali ya kutaka kuweza kupambana na majanga haya mawili UKIMWI pamoja na dawa za kulevya, naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu wameniomba nimweleze Mheshimiwa Waziri Jenista kwamba wamefurahi sana kufanya kazi na yeye, kwa sababu akija pale jinsi anavyopokea ushauri, tunashauriana mwisho mambo mengi wameyatekeleza kama Serikali, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze kwa sababu suala la UKIMWI na dawa za kulevya ni masuala mtambuka siyo ya Wizara moja, lakini nawapongeza pia Waziri wa TAMISEMI kwa kukubali sasa kwamba Kamati zile za UKIMWI ziweze kuingiza na madawa ya kulevya lakini pamoja na kutekeleza afua nyingine. Nampongeza sana pia Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa sababu kutokana na ripoti ya MSD ni kwamba dawa za UKIMWI zinapatikana asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Waziri wa Afya ni mchapakazi na mara nyingi tukimpa ushauri huwa anapokea tunakupongeza sana. Pia shukrani za pekee ziende kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, walikuja kwenye ripoti yao walikuja na Jeshi la Magereza kwa kweli hili Jeshi linatakiwa liigwe, Kamati tumefanya ziara Arusha, Manyara, Njombe na Iringa, lakini ukienda kwenye vituo vya kazi unakuta kwenye Halmashauri unaoneshwa wale watu wa hali ya chini ambao wametoka tu huko kwenye mitaa kwenye vijiji na kadhalika, lakini utaambiwa tu kuna watumishi wanapata hiyo lishe nini lakini hatujawaona watumishi ambao wamejitokeza wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walivyokuja Jeshi la Magereza ile ripoti yao karibuvituo vingi vya Magereza kuna watumishi ambao wamejitokeza wengine zaidi ya 100, ile inaondoa unyanyapaa hata wale wafungwa mahabusu wanajiona kwamba siyo wao peke yao hili suala ni la watu wote. Tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Kamati tunapenda kuwapongeza Wakuu wa Taasisi hizi mbili Tume ya Kudhibiti UKIMWI na Mamlaka ya Kudhibiti Madawa ya Kulevya, wanafanya kazi sana sana na wanapenda kuchukua ushauri, tunawashukuru sana. Kwa mfano, Mamlaka ya Dawa za Kulevya ni hivi karibuni tu kama sikosei Kamishna alianza kazi yake Februari, lakini ndani ya mwaka mmoja mambo yaliyofanyika katika kudhibiti dawa za kulevya ni makubwa mno utafikiri kama ni kipindi cha miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tuchukue suala ambalo lilisumbua muda mrefu vijana wetu suala la viroba, sasa hivi vijana wako vizuri, ajali zimepungua watu huko wanasema MB zinasoma sasa! Anajitahidi sana lakini wengi wamekamatwa, wengine wamekimbia, kidogo mambo yanaenda vizuri. Tunammpongeza sana, isivyokuwa kama tulivyoshauri Serikali sasa taasisi hizi mbili mzipatie fedha za kutosha za matumizi ya kawaida na za maendeleo ili waweze kuboresha mikakati yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Wajumbe wa Kamati kwa kazi nzuri, kwa kweli tunamshukuru sana Mheshimiwa Spika kwa sababu hii Kamati haijakaa muda mrefu, lakini sijui alitumia chujio gani kwa kweli Wajumbe walikuwa commited, walinipa ushirikiano mkubwa sana katika masuala mengi kuhakikisha tunaisaidia Serikali kuboresha mbinu mbalimbali kuhusu kupambana na masuala haya ambayo ni majanga ya madawa ya kulevya pamoja na UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi ni kwamba dawa za kulevya pamoja na masuala ya UKIMWI kwa kweli ni majanga ya Kitaifa. Serikali inaweza ikatoa hata trillions za fedha lakini kama sisi wenyewe hatutabadili tabia hizi fedha hazitasaidia lolote. Kwa hiyo, lazima tuanze na mtu mmoja mmoja lakini baadaye jamii na Taifa kwa ujumla ili tuweze kupambana na hili janga kwa sababu lina madhara mengi; vifo, yatima wanazidi kudorora kwa uchumi na kadhalika gharama kwa Serikali inaongezeka kama hivi wanatoa billions of money kununua ARVs au kununua hizi Methadone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru sana kwa Serikali kuweza kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya kupambana na janga hili la UKIMWI ingawa watu huko suala la unyanyapaa ni kubwa sana ndio maana inaweka usiri mkubwa kwa watu kutokupima afya zao. Kwa hiyo elimu ya kutosha inatakiwa kwa kweli itolewe ili watu waondoe ile dhana ya unyanyapaa, kujitambua na kuweza kupima na kutumia tiba ili itakapofika 2030, Tanzania iweze kufikia lile lengo la sifuri. Kwa hiyo, nawashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho labda niseme tu kama tip watu wengi wanasema kwamba mtu akitumia dawa muda mrefu basi hawezi kuambukiza, mimi niwaambie kwa sababu tulikuwa kwenye Kamati ya UKIMWI siyo kweli, ila ni kweli vidudu vinafubaa vinakuwa sio vingi, kwa hiyo chance ya kuambukiza inakuwa ndogo. Mimi siyo mtaalam sana lakini bado ukichukua damu yake na kadhalika unaweza ukapata UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kitu cha msingi wengi kwa mfano, Wachungaji anaenda kupima viral load vile vidudu vikiwa chini sana haviwezi kuonekana, wanasema not detected anawapeleka watu anasema unaona hakuna, mimi sina UKIMWI kumbe ni vichache kwenye viral load, akipima CD4 itaonekana kwamba ziko kwenye normal range, atasema unaona CD4 zangu mimi ni nyingi zinatosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipimo kizuri cha kuhakikisha na kujua huyu mtu ni positive au ni negative ndiyo hicho uende ukapime status ya kujua kwamba huyu mtu kinga yake ina- react kama ni positive au ni negative tusi-rely kwenye viral load na CD4 kwa sababu zile zitaonesha kwamba mtu hana lakini vile virusi anavyo ingawa ni vichache, kwa hiyo vikipata mazingira mazuri bado vitaendelea kusambaza UKIMWI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naliomba Bunge lako Tukufu sasa liridhie taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Kamati ya Masuala ya UKIMWI, maoni na mapendekezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika bajeti yetu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kweli kwa tukio hili ambalo linaendelea katika harakati zile zile za kutetea na kulinda maslahi ya Watanzania ili maslahi haya, rasilimali zetu ziweze kuwatetea na kuwasaidia hawa wanyonge hasa
akinamama ambao tuna shida ya afya na maji. Mungu ambariki sana Mheshimiwa Rais wetu achape kazi, tupo pamoja naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na Naibu wake kwa bajeti ambayo inatoa mwanga katika kumkomboa Mtanzania. Mambo hayawezi yakaja mara moja, ni taratibu, kwa hiyo, tuwape muda waweze kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza nijikite kwa kuondoa upotoshaji. Nimesikiliza michango mingi, upotoshaji ni mkubwa kwa kusema kwamba Marais waliopita na awamu hii wanaendeleza umaskini, kwamba wamechangia kulipeleka Taifa hili kwenye umaskini na Chama cha Mapinduzi ndiyo kinachangia katika kuletea umaskini Taifa hili. Siyo kweli, huu ni upotoshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niwaambie wananchi, maendeleo yetu hadi yanafikia hapa, bajeti zetu hazitekezwi; mara asilimia 38, mara asilimia 40 ni kutokana na matatizo mbalimbali ambayo yamelikumba Taifa hili tangu tumepata uhuru hadi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi tu napenda nieleze kwamba viongozi hawa, tukimchukulia Baba wa Taifa amejitahidi sana kulitoa Taifa hili katika umasikini; juhudi zake wote tunazifahamu, lakini amekumbana na vikwazo vingi; vikwazo vya nje na vikwazo vya ndani. Kwa mfano, wakati tulipoanzisha Azimio la Arusha tumeona wafadhili wengi sana waki-withdraw misaada kwa sababu ya sera zetu. Wajerumani walitoa misaada na Waingereza walitoa misaada. Kwa hiyo, bajeti iliyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya 1970, suala la oil bei yake ilikuwa kubwa sana. Export tulizotegemea zilishuka; kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, vita ya Kagera na mambo mengine yote hayo yameyumbisha uchumi. Wakoloni nao hawakutuacha huru, wakaendeleza ukoloni mambo leo; kila tunavyojitahidi kujikwamua na wenyewe wanatukwamisha. Kwa hiyo, haya yote yanachangia katika kufanya bajeti zetu zisiwe za kutekelezwa kiurahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya 1980 tukaachana na sera zetu, tukayumbishwa tena; tukaletewa zile sera za structure adjustment policies, tulikuwa hatutajiandaa ndiyo masuala ya ubinafsishaji, uwekezaji na hii mikataba mibovu ilipoanzia. Kwa hiyo, siyo kwamba ni mtu mmoja, ni timu ya wataalam mbalimbali. Wataalam hawa wanatoka wapi? Wanatoka kwenye vyama mbalimbali. Kwa hiyo, tusilaumiane, tuangalie tatizo ni nini? What is the root cause ambayo imetufikisha hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuangalie tutawezaje kujikwamua kwa haya Mataifa makubwa na sera zake? Sasa hivi tunashindwa kutekeleza malengo yetu, tunatekeleza malengo haya ya kidunia; ile Millennium Development Goals, sijui kuna ile 2030, yote haya yanaharibu. Tunashindwa ku- concentrate kuwaletea watu wetu mahitaji ya msingi, tunafanya mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zote hizi ni propaganda za Kizungu, lazima tuzitambue ili tuweze kuleta mshikamano katika Taifa letu. Wameshatugawanya na mambo ya vyama vingi, mambo ya NGOs na nini; yote hii ni divide and rule ili waweze kutuharibia. Kwa hiyo, Serikali inapopanga, huyu anakataa, huyu anafanya hivi, kunakuwa na mvutano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni matatizo ya ndani. Tumeona mambo ni mengi lakini rushwa na ufisadi ndiyo imetupelekea Taifa hili kufikia bajeti ambayo tunashindwa kuitekeleza. Pesa zinatolewa, miradi haitekelezwi, miradi hewa na Watumishi hewa, kwa hiyo, mambo yanakuwa mazito. Je, fisadi huyu ni nani? Fisadi huyu siyo wa Chama cha Mapinduzi peke yake; sio Rais wala siyo nani; ni sisi Watanzania hasa viongozi ambao tumepewa dhamana ya kuongoza Taifa hili kwa umoja wetu ndio tumefikisha hili tatizo katika mkanganyiko huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tufike mahali tujitambue. Hata kama wewe unakuwa kwenye Upinzani, hata kama wewe ni mwanaharakati, lakini kitu cha kwanza simamia maslahi ya Taifa hili, wasitugawanye. Kwa mfano, nilitegemea tungepongeza, maana wale wengine mnasema walikuwa wapole, walikuwa hivi; sasa tumempata Mheshimiwa Rais huyu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka Bunge la Katiba kila mtu aliyesimama alisema tunataka Rais atakayethubutu, Rais sio mwoga, Rais mzalendo na anayesimamia watu na wengine mpaka wakatumia Rais mwenye kichwa cha mwendawazimu, maana yake haogopi; Rais huyo tumempata, ndio Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Anafanya kazi kutetea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitegemea kwa mfano, juzi wakati anapambana na hili suala la madini ambalo limechukua trillions of money kwenda huko nje, nilitegemea Watanzania wote bila kujali itikadi zetu tungemuunga mkono. Hapa tunashuhudia Wabunge wengine wanaunga mkono na wengine wanakataa. Kwa nini? Kwa sababu tumeshagawanywa. Kwa hiyo, hali hii ikiendelea haitatuletea tija katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea wanasheria wa nchi hii wangeungana kumsaidia Mheshimiwa Rais ili kuweza kuiangalia upya hii mikataba. Hivi kama Mwanasheria anaweza akaungaunga aka-forge akamtetea yule muuaji kwa kutumia hizo sijui technical nini, kwa nini wasiungane ili kumsaidia Mheshimiwa Rais kutengeneza na kutetea haki zetu ambazo zimepotea na tunazidai? Badala yake tunaanza kubeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili Taifa mimi nasema tukifikia mgawanyiko huu kwamba kwa sababu Serikali hii labda ni ya Chama cha Mapinduzi, mimi niko huku, hatutafika na hizi ni mbinu na propaganda za mabeberu ili watugawanye waendelee kutunyanyasa na kuchukua rasilimali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wenzangu, tuamke tujitambue sasa ili tuweze kuhakikisha rasilimali zetu tunazilinda. Tanzania kwanza mambo mengine baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi sasa kwa upande wa bajeti. Bajeti yetu ni nzuri, kwa mfano suala la kumkomboa mkulima na tozo mbalimbali. Mimi nitazungumzia suala la kodi ya majengo. Nia ni kuondoa umaskini, lakini sasa kidogo nina wasiwasi pale ambapo malipo yamewekwa kwa flat rate ya Sh.10,000/= na Sh.50,000/= kwa nyumba ambazo hazijathaminiwa. Naomba kuuliza, je, hizi zikithaminiwa ina maana kodi itakuwa juu zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kuhusu nyumba za kuishi; leo mtu yupo kazini au amefanya biashara au leo ni Mbunge umepata mkopo ukatengeneza nyumba nzuri, baada ya hapo huna kazi, biashara ilikufa halafu nyumba ile sasa imethaminiwa ulipe labda Sh.300,000/= auSh.400,000/=. Hii itaishia kwamba huyu mtu atanyang’anywa ile nyumba kwa sababu ile nyumba haizalishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali, nyumba za kuishi zote, contribution ni lazima katika kuleta maendeleo; iwepo labda hata kati ya Sh.2,000/= kwa zile ambazo vigezo vyake ni vya chini, labda mwisho iwe ni Sh.50,000/= ili watu waweze ku-afford. Otherwise tutaenda tu kuuza nyumba za hawa wananchi ambao sasa hivi kazi hakuna. Unasema huyu ana mtoto, watoto wenyewe kazi hawana, tunao majumbani. Kwa hiyo, tutaishia kuendeleza umaskini. Bora mtu awe na nyumba yake, asubuhi anajua akagange vipi. Kwa hiyo, naishauri Serikali hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala maji ni muhimu sana katika ku-stimulate maendeleo, kwa hiyo, tunaomba sana, akinamama na watoto wetu wa kike wananyanyasika, wanapigwa, wanabakwa na ndoa zinavunjika kwa sababu ya maji. Kwa hiyo, naiomba Serikali, bajeti ya maji hii na nawaunga mkono wenzangu kwamba ile Sh.50/= iongezwe ili akinamama waondolewe hii adha, kwa sababu pia watapunguziwa muda. Time factor ni muhimu sana katika suala la maendeleo. Watapata maji jirani, lakini watafanya na shughuli nyingine za uzalishaji na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la mazingira. Suala la mazingira linatu-cost sana katika nchi yetu hii. Wote tunashuhudia mazingira sasa hivi yanaharibiwa mno. Tunaiomba Serikali ihakikishe kwamba… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Job Yustino Ndugai kwa Uamuzi wake wa Kulifanya Bunge Kutekeleza kwa Vitendo Dhana na Bunge Mtandao (e-Parliament)
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu katika kumpongeza Mheshimiwa Spika kwa maamuzi mazuri ya kutekeleza ahadi yake ambayo binafsi nilifikiri labda tunaishia hivihivi bila ya tablets au bila ya kuwa na e-Parliament. Tunashukuru sana kwa sababu sasa katutoa kwenye analojia tunarudi sasa kuwa Wabunge wa kidigitali zaidi. Kama walivyozungumza wachangiaji wenzangu kwa kweli, tutaokoa pesa nyingi lakini pia itasaidia suala zima la utunzaji wa siri na katika kutunza kumbukumbu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Spika kwa uzalendo wake. Kama tulivyoona tumetumia wataalam wetu wa ndani. Watu wengi wanasema degree za Tanzania haziajiriki, hazina mshiko, jamani hawa ni watu ambao wamesomea utaalam nchini kwetu na ndiyo wanatumika. Kwa hiyo, kwa uzalendo huu tutaokoa pia pesa nyingi kwa ajili ya matengenezo na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kweli, naungana kwa dhati kabisa na wenzangu kumshukuru sana Mheshimiwa Spika, nampa hongera sana kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanya. Ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipatia nafasi ili niweze kuchangia katika bajeti yetu hii. Kwanza kabisa niungane na Waheshimiwa Wabunge wote waliotangulia kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri wake na timu nzima ya Wizara hii ya Fedha kwa kazi nzuri wanayoifanya hasa katika kutatua changamoto zinazohusu makundi mbalimbali, wafanyabiashara wakubwa na wadogo lakini na makundi ya wakulima kwa kutoa tozo mbalimbali ambazo zilikuwa ni kero kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na suala la muda, napenda nijielekeze hasa katika mambo mawili; kwanza nijikite katika idara yangu ya vyuo vikuu lakini baadaye nitajikita kwenye bajeti kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa wetu Rais mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli katika kushughulikia masuala ya chuo kikuu hasa katika utoaji wa mikopo ambao mwaka hadi mwaka bajeti yake inazidi kupanda. Kwa mfano, mwaka jana takribani wanafunzi 123,000 walipata mikopo na bajeti hii ya 2019/2020 takribani wanafunzi 128,000 wataendelea kupata mikopo takribani bilioni 450, tunapongeza sana Serikali yetu kwa juhudi hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, kwa nia njema kabisa mikopo hii inalenga katika kuhakikisha makundi yote ya watoto wa Tanzania wakiwemo wakulima, wafanyakazi lakini hasa wale wa kipato cha chini wanaweza kushiriki katika kutengeneza wataalam mbalimbali katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ombi langu moja kwa Mheshimiwa Waziri, mikopo hii pamoja na uzuri wake lakini kuna changamoto ambazo zimejitokeza hasa ukiangalia sasa jinsi ilivyoboreshwa kweli mwanzo watu walisuasua lakini baadaye wakatafuta namna ya ulipaji wa mkopo. Mkopo huu unatakiwa mwanafunzi anapomaliza chuo alipe baada ya miezi 24 lakini alipe kwa asilimia 15 lakini pamoja na hiyo kuna hiki kipengele cha Value Retention Fund. Sasa kwa kufuata vigezo hivi, inafanya huu mkopo sasa badala ya kumsaidia huyu mtoto wa maskini imekuwa sasa ni mzigo mkubwa sana hasa kwa sababu ya hii Value Retention Fund.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kijana ambaye amemaliza chuo kikuu mwaka 2015, kama utatoa hii miezi 24 maana yake unahesabu 2016 na 2017, yupo kwenye grace period, ina maana unahesabu 2018 na hii 2019 kidogo. Kijana huyu juzi wakati anakwenda kuangalia anadaiwa shilingi ngapi, kwa sababu ya hii Value Retention Fund; huyu kijana alikopeshwa milioni 10 lakini alivyokwenda kucheki juzi amekuta anadaiwa milioni 16.5. Sasa je huu mkopo kweli nia yake ile njema imetolewa sasa imekuwa kama ni business ambayo kwa kweli itaathiri kwa kiasi kikubwa sekta hii ya chuo kikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri aliangalie hili suala kuweza kurekebisha kama vile tulivyofanya ile quick appraisal kwenye tozo ya kodi ya pedi. Kwa hiyo, hivi nayo sasa wafanye evaluation kwamba huu ulipaji kwa kweli utamsaidia mtoto wa mtanzania au vipi. Kwa hiyo, hilo ni ombi langu kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na asilimia 15 naomba tena nirudie bado ni kubwa mno. Hii sasa implication yake itakuwa kwamba wanafunzi sasa wameshaanza kuambizana burden ya huu mkopo, matokeo yake itafika mahali wakati ule Pride, Finca walitoza kodi kubwa sasa hivi zimepotea baada ya watu kutafuta vyanzo vingine. Kwa hiyo, tunaweza tukakosa hata wanafunzi wa kuchukua mikopo au kozi zile ambazo zinahitaji kusomewa muda mrefu hasa za sayansi, zitaathirika vibaya wanafunzi hawataenda kusoma kule kwa sababu ya huu mzigo ambao umeongezwa na hii Value Retention Fund. Kwa hiyo, naomba sana tuangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja hayo, ninaomba niseme kwamba hawa vijana alipe asilimia 15, mkopo ambao haumaliziki mpaka anazeeka, inaweza pia hata kichocheo kwa upande wa ufisadi na rushwa ambayo Mheshimiwa Rais wetu kila siku anapambana na ufisadi na rushwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, ninaomba kwamba Serikali itoe zile fedha ambazo zimeahidi katika kujenga hosteli. Juzi tumepoteza binti yetu wa kike ambaye alivamiwa na majambazi wakati anakwenda. Kwa hiyo, hosteli zikijengwa ndani ya chuo, zikawa na ulinzi mkuu, itasaidia sana kuepusha madhara kama haya tuliyoyapata hivi karibuni.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niingie sasa kwenye suala la sera mbalimbali katika nchi yetu katika kukuza uchumi wa nchi yetu. Wengi tumeangalia suala la sera ya huduma bure, sasa huduma bure katika jamii kwa mfano naipongeza sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kuwa sikivu kwa kuweza kuwasaida wanyonge katika kupata huduma mbalimbali. Kwa mfano, tayari tuna Sera ya Huduma Bure kwenye elimu bure, watoto, wajawazito na wazee wanatibiwa bure lakini hata kwa magonjwa ya kansa bure. Kwa hiyo, Serikali imejaribu kupunguza mzigo mkubwa kwa wazazi ili waweze kupeleka watoto wao shule. Pia kuna mpango mzuri wa TASAF ambao unasaidia watu maskini waweze kuwasaidia hasa kwa upande wa mtoto wa kike.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, sasa hivi kuna hii debate inayoendelea kuhusu taulo za kike. Ni wazo zuri sana lakini tuangalie je uwezo wa uchumi wetu, hivi tutaweza kweli kila kitu bure, tayari Serikali jamani imeshatoa mpango wa TASAF. Sasa TASAF package mojawapo ni kumsaidia hata huyu mtoto wa kike kupata taulo. Hata hivyo, tuangalie je, kigezo cha kwamba mtoto anapokuwa kwenye mzunguko wake ule wa mwezi, je, tukitoa hii taulo bure tayari inaweza ika-solve problem?

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge, nafikiri kipaumbele tungewekeza kwenye vyoo na maji. Huyu mtoto anaweza akapata taulo lakini kama shule haina choo, hawezi kwenda shule lakini shule kama hakuna maji hawezi pamoja na kwamba ana taulo atabaki nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ndugu zangu, tukiangalia ukisoma kweli kuna nchi zimeweza ku-implement haya masuala ya taulo lakini wameangalia the needy people siyo the whole population watoto wa kike wote kama ilivyokuwa elimu bure hata mtu mwenye uwezo basi umlipie. Tuangalie ni familia zipi kweli hazijiwezi lakini tayari kuna mpango wa TASAF ambao umeshasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri tujielekeze sasa kwenye masuala yale ya msingi, tuelekeze suala letu la vyoo, maji na afya kwa sababu huyu mtoto anaweza akawa kwenye mzunguko wa mwezi lakini anaumwa tumbo, atahitaji apate panadol na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tujielekeze kwenye masuala ya kimaendeleo, tuache hivi vitu bure bure kwa sababu ukiangalia sana, dunia ya leo kuna watu watapitia kwenye mgongo wa demokrasia, usawa wa jinsia na harakati za binadamu kutengeneza maslahi yao binafsi. Uchumi wa nchi yetu bado ni wa chini hatujafikia hata uchumi wa kati, hatuwezi kila siku tunatoa kitu burebure, je, nafasi ya mzazi naye katika kuchangia familia yake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia sababu zinazofanya Afrika ziwe maskini mojawapo ni uvivu pamoja na poor policies. Poor policies maana yake siyo kwamba ni policy mbaya lakini una-implement sera ambayo siyo wakati muafaka kwa wakati huo. It’s not a bad policy lakini it’s a poor policy. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano sasa hivi unasema kila kitu bure, Waheshimiwa Wabunge ninyi ni mashahidi kila siku mnasema bajeti haitimii, hakuna bajeti hata siku moja ikafika asilimia 100, leo unataka uongezee tena Serikali eti ikatoe tena pedi bure kwa watoto wa kike, fedha zitatoka wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nafikiri kwa Serikali katika kusaidia mpango wa TASAF, katika kusaidia elimu bure, mzazi naye aendelee kuchangia katika kumlea huyu mtoto ili sasa tujielekeze kwenye mipango hii ya maendeleo. Mwanamke anahitaji maji na afya ili tuweze kutekeleza mipango hii ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme ukweli pamoja na nia nje, lakini hatujafikia bado wakati muafaka wa kufanya kila kitu burebure, hii sasa ni kuingizana mkenge ili kesho na keshokutwa waje tena watugeuzie kibao ooh mlipanga hivi; nasema hizi zote ni political pressures.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia Uganda waliibeba hii ajenda ya pedi bure, ukiangalia Kenya, South Africa kwa nini zote zitokee kwa wakati mmoja; tunajua strategies hizi za watu. Wanajua sasa hivi tuna wataalam, tutawekeza, tutafanya maendeleo wanaturudisha nyuma, wewe kila kitu utoe bure ile hela haizalishi maana yake nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa leo niliamua nijikite hapo, nashukuru sana kunipa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii.

Kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake kwa kazi nzuri wanazozifanya lakini pongezi za pekee zimuendee Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama yetu Mheshimiwa Samia kwa juhudi kubwa sana anazozifanya katika kuifanya Tanzania kuwa ya kijani. Kwa hiyo, tuendelee kumuunga mkono, tunamuona katika upandaji wa miti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juhudi hizi za mama yetu naona kama vile zinakinzana, yeye anasema tupande miti na miti inapandwa, lakini kuna uharibifu mkubwa sana wa mazingira, wengine wanaendelea kukata miti. Nitolee mfano kwenye Mkoa wangu wa Morogoro katika Halmashauri ya Morogoro, ile Milima ya Uluguru ndiyo chanzo kikubwa sana cha maji, lakini ukiangalia kwenye ile milima ambapo kulikuwa hakuna shughuli ya kibinadamu inafanyika lakini sasa hivi kuna ujenzi holela. Ukiangalia milima ile ya Bigwa, Kigurunyembe kuelekea Pangawe, ujenzi unaendelea tena wa nyumba za nguvu, nani anatoa vibali na hawa watu wanachukuliwa hatua gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Morogoro leo tunakunywa maji ya chumvi? Kwa kweli, haikubaliki. Kwa hiyo, tunaomba juhudi hizi za Serikali ziungwe mkono mpaka huku kwenye halmashauri zetu maana ndiyo kwenye watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kitu kingine niseme uharibifu wa mazingira unasababishwa pia na shughuli za kiuchumi na maendeleo ya binadamu. Hatuwezi tukazuia maendeleo, lakini tunatakiwa tuwe na sustainable development. Kwa hiyo, kila aina ya maendeleo inayofanywa basi lazima tuhakikishe maendeleo haya yanakuwa rafiki kwa mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumza kuhusu suala la Stiglers’ Gorge, hii haikwepeki, tunajua matatizo ya umeme ambayo tunapata katika nchi yetu na tunasema Tanzania ya viwanda lazima tuwe na umeme ambao ni sustainable. Ombi langu ni kwamba ile tathmini iliyofanywa (environmental impact assessment) vile vitu vizingatiwe ili isije ikaleta madhara, lakini mradi una umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine nizungumzie uchafuzi wa mazingira ambao umekithiri na sasa hivi unatuletea madhara makubwa sana nchini. Tumeona mafuriko Dar es Salaam, Morogoro, Mwanza, Arusha, kila sehemu, lakini tatizo kubwa hapa ninaloliona mojawapo ni taka ngumu hizi ambazo ni product za plastic bags pamoja na chupa. Kama Serikali tulifanya mkakati wa makusudi kuweza ku-ban viroba ambavyo pia vilichangia kuharibu mazingira lakini hata afya za watu, kwa nini tusifanye mkakati huo huo katika ku-ban uzalishaji wa plastic na matumizi haya ya plastic kwa sababu inaleta madhara makubwa sana kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapata hasara, hivi ukiangalia kodi inayopata kwa vile viwanda na gharama inazopata ambapo wananchi wanapata hasara ya mali zao, magonjwa, miundombinu, hivi tukifanya cost benefit analysis, kweli hii plastic ina tija katika nchi yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie kizazi cha leo na cha kesho kwa sababu inatengeneza pollution. Sasa hivi mito mingi Dar es Salaam huwezi ukanywa maji, inakuwa depleted. Maji hayatumiki, ardhi itafika mahali haitumiki, hewa yetu itakuwa haitumiki, sasa kitu kisipotumika maana yake kinakuwa depleted. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haya mazingira Mheshimiwa Waziri, pamoja na mikakati hii utekelezaji sasa ndiyo unaotakiwa kwa sababu, madhara, vyanzo, tumeshavijua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kitu kingine niseme kuhusu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Spika, na mimi napenda kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa pongezi kwa Serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wa Mheshimiwa Raisi wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kuhakikisha Watanzania wanaishi kwa amani na utulivu na kuendelea kusimamia kutekeleza Ilani ya CCM kuwaletea wananchi maendeleo endelevu.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na hotuba nzuri iliyojaa matumaini ya kufikia malengo yetu ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kukupongeza kwa kazi nzuri na weledi wa hali ya juu kuhakikisha vikao vya Bunge la Bajeti vinaendelea kwa kuchukua tahadhari zote zinazotakiwa katika kujikinga na ugonjwa wa mapafu ujulikanao “Covid-19”. Nakupongeza pia kwa jinsi ulivyoendelea kuimarisha matumizi ya Bunge Mtandao ambao umeendelea kurahisisha vikao, lakini pia kupunguza gharama kubwa hasa ya kuchapisha marejeo mbalimbali.

Baada ya pongezi hizo naomba sasa kuchangia kwa kutoa ushauri kuhusu Mfuko wa UKIMWI (ATF).

Mheshimiwa Spika, bajeti ya UKIMWI inategemea kwa zaidi ya asilimia 90 fedha kutoka kwa wafadhili wa nje. Lakini tumeshuhudia wafadhili hawa wameanza kutuwekea masharti ambayo hayaendani na utamaduni wetu na kutishia kuondoa ufadhili kwenye suala la UKIMWI. Lakini pia tunashuhudia nchi zote duniani sasa zikiyumba kiuchumi kutokana na shughuli nyingi za kiuchumi kusimama kutokana na ugonjwa huu wa corona. Kwa mantiki hii, tunategemea kuona wafadhili wakijitoa katika kufadhili miradi mingi ya maendeleo ikiwemo ya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, UKIMWI bado ni tatizo na janga la kitaifa na dunia. Hivyo basi, naungana na wote walioshauri Serikali kuwa ni wakati muafaka sasa kama nchi kuchukua tahadhari mapema kwa kutafuta tozo maalum kwa ajili ya mfuko huu wa UKIMWI. Asilimia 4.7 ya maambukizi kitaifa bado ni kubwa na tishio, hivyo tutoe kipaumbele kwa mfuko huu kuhakikisha tunapata chanzo endelevu cha fedha kwa ajili ya ATF.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda kutoa pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuipa kipaumbele sekta ya afya na kuendelea kuboreshwa kila wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi sana kwa mafanikio ambayo yanasaidia wananchi wa Tanzania kupunguza gharama za matibabu hasa nchi za nje. Mafanikio haya ni kama vile huduma za kupandikiza figo Muhimbili na Benjamin Mkapa Hospital; chanjo muhimu kwa watoto, chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi kwa wasichana; upatikanaji wa dawa kwa kiwango kikubwa; dawa mpya ya kifua kikuu kwa watoto na ununuzi wa vifaatiba, mashine na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, juhudi hizi zinalenga kuendelea kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma za afya kwa wakati na ubora zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi pia kwa Mheshimiwa Waziri wa Afya pamoja na Naibu Waziri wake na timu yote ya wataalamu kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kusimamia na kutekeleza majukumu yao na kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kutoa ushauri kwa Wizara hii ili kuweza kuendelea kutoa huduma bora; kuendelea kutoa elimu kwa jamii ili wawe na tabia ya kupima afya zao na kugundua matatizo kabla hayajawa sugu na kuwasababishia vifo, gharama kubwa za matibabu na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, elimu zaidi itolewe kupima tezi dume, saratani, ugonjwa wa ini, magonjwa yasiyoambukizwa (non-communicable diseases).

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza juhudi za Serikali kuwa na Bima ya Afya kwa kila mwanachi. Hivyo ili kuondoa changamoto ya msongamano wa wagonjwa kumuona daktari na kufanya vipimo ni vema sasa Serikali ikaendelea kuajiri madaktari na wasaidizi wengi wa afya ili kuondoa adha hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kitengo cha Tiba Asili ni cha muda mrefu, lakini bado hatujaona ripoti inayoonesha mafanikio ya upatikanaji wa dawa zilizothibitishwa na kitengo hiki ili zisambazwe kwenye maduka ya dawa. Hii itasaidia kupunguza matumizi ya dawa zenye kemikali ambazo si nzuri sana kiafya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuendelea kuboresha Hospitali za Rufaa za Mikoa kwa kuweka mashine za kisasa kama vile MRI, X-ray (Digital); CT-SCAN na kadhalika, lakini pia kuajiri Madaktari Bingwa ili kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Muhimbili na kupunguza gharama za usafiri na malazi kwa mgonjwa na ndugu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa kuna wanawake wengi wanaojifungua watoto zaidi ya mmoja. Wapo hadi wanaojifungua watoto watano. Wote tunafahamu ugumu wa kulea mapacha au idadi kubwa hiyo ya watoto watatu, wanne, watano na kadhalika. Ili kuokoa maisha ya watoto hawa pamoja na mzazi, kunahitajika matunzo ya hali ya juu ukizingatia familia hizi vipato vyao ni vidogo kukidhi kulea watoto wanne (kwa mfano) kwa wakati mmoja. Je, Wizara ina mpango mkakati gani katika kusaidia familia hizi kulea hawa watoto angalau katika kipindi cha mwaka mmoja wa kwanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, watoto wa mitaani na mimba za utotoni ni tatizo linaloendelea kukua katika nchi yetu. Sababu za watoto wa mitaani na mimba za utotoni zipo nyingi, lakini sababu mojawapo ni baba wa watoto hawa kukataa kutoa malezi na matunzo, hivyo kupelekea mama zao kushindwa kuwapa mahitaji ya msingi ikiwemo elimu, afya, chakula na kadhalika. Hali hii husababisha watoto hawa wajitafutie riziki kwa njia mbalimbali zikiwemo kuombaomba mtaani, kujiingiza katika mapenzi wakiwa na umri mdogo na kutumia ngono zembe na kadhalika.

Je, Serikali sasa, ina mpango mkakati gani wa kuhakikisha baba wa watoto hawa wanawajibika kulea watoto wao, maana hivi karibuni tumeshuhudia akina mama walivyofurika kwenda ofisini kwa Mheshimiwa RC wa Dar es Salaam kupeleka malalamiko yao. Hali hii imeonesha/
kudhihirisha kuwa kuna tatizo katika vyombo vya maamuzi ikiwemo Mahakama na Ustawi wa Jamii katika kuwawajibisha akina baba hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii ya kuchangia na ninaomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Elimu. Niungane na Wabunge waliotangulia kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Watendaji wote katika Wizara hii ya Elimu kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya, bila kigugumizi tunaona mabadiliko makubwa ambayo yanatokea katika sekta yetu ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mingi tulikuwa tunalia na hizi shule kongwe Kilakala, Ilboru na zingine, mmeweza kuzikarabati ili sasa ziweze kuendelea kutoa elimu nzuri na mazingira mazuri kwa wanafunzi wetu tunashukuru sana. Pia katika usimamizi wa elimu bure kwa wanafunzi wetu shule ya msingi kuanzia Darasa la Kwanza mpaka form four tunapongeza sana Serikali. Pongezi kubwa ziende kwa Mheshimiwa Rais kwa kuweza kupitisha sera hii ya elimu bure moja kwa moja pale alipopata uongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nizungumzie zaidi na nijikite kwenye suala la ubora kwa sababu ukiangalia taarifa zote mbili, Wizara pamoja na taarifa ya Kamati zote kwa kweli kwa masikitiko inaonesha ubora wa elimu hasa shule za Serikali jinsi ubora wa elimu unavyozidi kushuka ndiyo maana watu hapa wanafanya comparison kati perfomarnce ya shule za private na shule za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuwapongeza sana wadau wa shule za private wanafanya kazi kubwa sana, wanalenga hata fursa na soko la dunia hii linaendaje, hasa niwapongeze kwa kuweza kuipa kipaumbele lugha ya kiingereza katika taaluma. Kwa sababu hapa tunazungumzia lugha sawa kiswahili ni yetu lakini tunapozungumzia taaluma kwa sababu hii lugha ina mambo mengi ambayo ninaweza nikaeleza baadae. Nawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la ubora ubora huu wengi tumezungumzia hii performance, kuna factors ambazo zinafanya mwanafunzi afaulu, mioundombinu, walimu wa kotosha, motisha kwa walimu participation ya wadau mbalimbali wakiwemo wazazi, wanafunzi na lugha ya kufundishia, hivi ni vitu muhimu sana katika sekta hii ya elimu, lakini upande wa shule zetu za Serikali hizi factors zote zinasuasua zinayumba na ndiyo maana shule za private zina perfomance nzuri kwa sababu miuondombinu ni mizuri ya kufundishia, walimu wapo wa kutosha, motisha kwa walimu ni imporntant factor katika kufanya elimu bora wanapata, pia wazazi wako karibu sana na wanafunzi wao.

Ukiangalia kama walivyosema wachangiaji wengine hawa wanachukua wanafunzi wale cream ndiyo wako pale. Halafu na lugha ya kufundishia hao wanaanza toka chekechea mpaka form four wanatumia lugha ya kiingereza na ili mtu aweze kueleza ideas zake lugha ni muhimu sana, shule zetu za Serikali hivi vitu tuna-miss. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ushauri wangu ili shule za Serikali uonekane unafanya kazi boresheni miundombinu ya kufundishia. Sasa hivi tumeingia kwenye suala la elimu bure miundombinu haiko tayari, tatizo letu tunaanza ku-implement sera na kuifanyia kazi kabla ya maandilizi, hii ni changamoto kubwa sana kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano sasa hivi unasema watoto waishie darasa la sita mmefanya utafiti gani, mmewaandaa hawa watu kwa kiasi gani, mnachukua walimu wa sekondari mnawapeleka kufundisha Shule ya Msingi kweli wanafaa? Hivyo, hizi changamoto mzifanyie kazi ili siku moja na shule za Serikali tusimame kidedea. Ingawa kwangu nasema nakumbuka maneo ya Mwalimu Nyerere wakati anazungumza nchi matajiri na sisi ambao siyo, anakuambia unamchukua mtu wa heavy weight unaenda kumshindanisha na huyu wa featherweight haiwezekani huyu mwenye heavyweight atamshindwa. Kwa hiyo, hizi shule za private unazishindanisha na shule za Serikali moja kwa moja kati ya watu 100 Serikali itakuwa nne kutokana na ubora wa miundombinu na changamoto nyingine. Kwa hiyo Serikali muweze kuboresha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine nizungumze suala la lugha, kwamba lugha ni tatizo katika shule zetu. Mwanafunzi anaanza shule za Serikali zilizo nyingi kiswahili hadi darasa la saba, form one anaenda kiingereza hawezi kufanikiwa. Kwa hiyo, lazima tuchague lugha ya kiingereza ni rahisi kutengeneza vitabu vya kiada kuliko kule Chuo Kikuu. Chuo Kikuu ili mtu awe daktari alisomee sikio kwa wale ambao wamesoma degree mpaka Ph.D huko huwezi ukafanya utafiti kwa kutumia text book, unahitaji reference na bibliography, sikio lina vitabu zaidi ya 1,000 sasa wewe ukisema leo kwenye taaluma ukaweke lugha ya kiswahili hapana, hatutafika na fursa za dunia tutazikosa. (Makofi)

Mshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kwa upande wa Vyuo Vikuu, nakupongeza sana suala la mikopo lilikuwa tatizo sasa hivi umejitahidi wanafunzi wetu wanaendea vizuri. Kwa hiyo, ninaomba sana kwa upande wa vyuo vikuu uweze kuboresha mambo yafuatayo:

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bima ya Afya kwa wanafunzi wa vyuo vikuu, wanafunzi wanapofika term ya kwanza semester ya kwanza wanalipa zile fedha za bima, lakini baadae wanakuja kuipata semester ya pili, kwa hiyo, naomba uboreshe hiyo. Pia suala la kuhama chuo kutoka chuo kimoja kwenda chuo kingine bado mfumo hauko vizuri muufanyie kazi, kwenye mikopo ninataarifa kwamba wanafunzi 35 wa DIT wamepunguziwa ile ada ya mikopo kumetokea nini, badala ya shilingi 900,000 wanalipiwa shilingi 600,000 kumetokea nini? Mnawa-frustrate hawa wanafunzi. Vilevile muendeleze miundombinu kama hostel za wanafunzi ili kuwaokoa hawa... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu. Kwa upande wangu, mara nyingi nasema Wizara hii ya Utamaduni ni Wizara mama ya Wizara zote ambazo zipo kwa sababu ndiyo Wizara ambayo inajenga misingi ya utaifa wetu ikiwemo uzalendo, maadili, udugu, mshikamano na ujamaa wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kweli niwapongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake wote akiwepo Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kuifanya ili kuweza kufikia malengo ya maendeleo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujikita sehemu kubwa moja ambayo kwa kweli bila kukumbushana maendeleo yote tunayoyapanga, bajeti yote tunayoipitisha katika Taifa letu haitaweza kufikiwa kama Watanzania leo hatutakuwa kitu kimoja na wazalendo katika nchi yetu. Tumeona mifano mingi ambayo inaendelea katika Taifa letu ambayo kwa kweli uzalendo wetu tusipoendelea kujikumbusha nchi hii itagawanyika katika misingi ya ukabila, udini, vyama vingi na kadhalika na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi dunia tunaona imeingia katika crisis ya uchumi, kwa hiyo, kila mtu anatafuta namna ya kumtawala mwingine ili aweze kupata masoko na kujua rasilimali zitatoka wapi. Watanzania tusipokuwa na mshikamano katika uzalendo na utaifa wetu kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu mpendwa kwa kazi anazozifanya hatutaweza kufikia maendeleo hata tungekuwa na Wizara ngapi au bajeti kubwa kiasi gani. Kwa sababu uzalendo ndiyo ambao unasema Taifa kwanza halafu mimi baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niombe kwamba fedha zote walizoomba Wizara hii wapewe lakini pia hata zile zilizobaki za 2017/2018 wapewe katika misingi niliyoisema ya umuhimu wa Wizara hii. Kwa nini nasema hivi? Kwa mfano, katika katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 18, item ya 31 na ukurasa 24, item ya 42 amezungumzia suala la uzalendo. Sasa uzalendo maana kama nilivyosema nchi kwanza mengine baadaye, tumeona sasa hivi nchi inaweza ikawa na amani na utulivu lakini bila uzalendo maana yake rasilimali za nchi hazitatumika kwa tija ya Taifa zitatumika kwa mtu mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nisisitize kwamba katika nchi yetu kuna vipengele vya uzalendo. Vijana wengi sasa hivi wamechukua madaraka lakini wamezaliwa katika kipindi cha mageuzi, miaka ya 80 kuja mbele wakakutana na sera za ubinafsishaji, vyama vingi, haki za binadamu, kwa hiyo, kama alitoka kwenye familia ya ufisadi na uhujumu anachokijua ni hiko. Kwa hiyo, Wizara hii ina jukumu kubwa kushughulikia suala hili. Mlizindua Kampeni ya Uzalendo nafikiri 2017, nilikuwa nategemea katika ripoti yenu hiki kipengele jinsi ya kuwalea hawa vijana kuanzia mtu anapozaliwa, uzalendo ndugu zangu unazaliwa, unakua na unaweza ukafa. Kwa hiyo, lazima tulinde misingi ya uzalendo ambayo waasisi wetu walituwekea. (Makofi)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Tisekwa kuna taarifa, Mheshimiwa Sophia Mwakagenda.

T A A R I F A

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumpa taarifa Daktari kwa kile anachokichangia na mimi namuunga mkono. Hata hivyo, nataka kumwambia uzalendo unaanzia kwenye nyumba hii hii ambayo ndiyo tunatunga sheria. Kwa hiyo, nakubaliana naye kwamba uzalendo unaanzia humu ndani ndiyo utafika nje. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Jasmine Tisekwa, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru anatambua kwamba wote tunatakiwa tuwe wazalendo kuanzia kwenye nyumba hii. Pale tunapotunga sheria wote tukae ndani ya nyumba hii tutunge sheria, tunapopitisha bajeti wote tukae tupitishe bajeti kwa umoja wetu kwamba ndani ya nyumba hii hoja ndiyo zishike mshiko na siyo vitendo vya kususa na kadhalika. Kwa hiyo, nashukuru kwa kulitambua hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niseme kwamba kuna Tunu zetu za Taifa ambazo zimejenga uzalendo nchi hii. Kwa mfano, Uhuru, Muungano na Mwenge wa Uhuru. Hivi vitu lazima watoto wetu wanapozaliwa, kama nilivyosema uzalendo toka mtu anapozaliwa kwa sababu unazaliwa na unakua, hizi tunu tunatakiwa tuzienzi lakini leo hii Uhuru, Muungano na Mwenge wa nchi hii unaonekana kama wa chama fulani. Kuna wenzetu bado wanadai Uhuru, kuna watu ambao wanataka Muungano uvunjike, kuna watu ambao wanataka Mwenge wa Uhuru usitishwe lakini hivi vitu vimebeba philosophy kubwa ya mshikamano, udugu, utaifa wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nashauri Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na Waziri nyingine Mwenge wa Uhuru uheshimiwe kitaifa, bajeti yake iende kwenye Taifa isiwe sasa kuomba kama ilivyo sasa kwa sababu tunapoomba watu wanafikiri labda hii ni ya kichama lakini ndani ya Mwenge wa Uhuru ndiyo tunasema imulike, ilete amani, upendo na umoja. Kwa hiyo, naomba Kampeni hii ya Uzalendo mwende kule chini kuanzia chekechea mpaka vyuo vikuu tujenge taifa la uzalendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kusema hayo kwa mfano sasa hivi, Serikali yetu ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kuna miradi hii mikubwa, mimi nimesomea maendeleo, kuna stimulus za maendeleo ambazo ni usafiri wa uhakika lakini pia energy (umeme) wa uhakika. Nachukulia mfano hii Stigler’s Gorge, kwanza neno Stigler lenyewe limetoka wapi, huyu ni mkoloni, upembuzi yakinifu wa hii Stigle’rs Gorge ilifanywa toka wakati wa ukoloni na walikubali. Je, hili bwawa kwa mfano lingejengwa wakati wa ukoloni haya masuala ya mazingira wangeyazungumza? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli katika Awamu hii ya Tano hii Stigler’s hakuianza yeye ni strategic plan ya miaka toka ya ukoloni, ndugu zangu tuwe wazalendo. Ulaya na Amerika wameharibu mazingira kiasi gani? Leo umeme tunalipa senti 12 wenzetu wanalipa senti 0.0 something, hivi hatuoni? Kwa hiyo, suala la uzalendo ni muhimu sana kulijenga katika nchi yetu, tumuunge mkono Mheshimiwa Rais kwa maendeleo ya nchi yetu, tusipokuwa wazalendo tutakuwa wabinafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nimejikita kwenye sekta ya uzalendo na utaifa. Uzalendo hauwezi ukaja kwa kuzungumza lakini nachotaka kuzungumza pia rushwa, ufisadi, uonevu, dhuluma, hivi vyote vinamong’onyoa msingi wa uzalendo. Kwa hiyo, wenzetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Daktari, muda wako umekwisha.

MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, oooh, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii muhimu ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Niungane na Wabunge wote ambao wamewapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Naibu Katibu na Watendaji wote pamoja na Wakuu wote wa Taasisi wa Wizara hii kwa kweli kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa unyenyekevu na usikivu wako. Kwa jinsi ninavyokufahamu, kwa kweli ukisikiliza hii taarifa imesheheni na umetumia ile smart approach kwamba unasema nitafanya nini kwa muda gani, kwa hiyo, ni rahisi hata kuwa measurable tutaweza kukuuliza mbona ulisema hiki kuliko zile tulizozoea kwamba tukipata fedha, tukifanya hivi ndipo tutafanya; lakini umeonyesha. Kwa mfano, kuanzia page 134 – 213 imesheheni mambo gani yatafanyika. Hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama Mwakilishi wa Vyuo Vikuu nimekaa na Uongozi wa Serikali ya Wanafunzi pamoja na Viongozi wa Academic Staff takribani vyuo 10 hivi, wamenituma kwamba upeleke salamu kwa Mheshimiwa Rais wetu kwamba wana imani na Mheshimiwa Rais wetu pamoja na wasaidizi wake wote akiwemo Mheshimiwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu jinsi wanavyotekeleza mipango ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wanasema wanapongeza sana, lakini vijana wa Vyuo Vikuu wanashukuru sana kwamba mikopo sasa hivi inapatikana kwa wakati pamoja na kwamba kuna changamoto za hapa na pale, lakini wana-support sana zoezi lile la vyeti feki. Wakifikiria jinsi wanavyo-toil halafu mwingine anapata cheti feki anapata kazi. Kwa hiyo, wanampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa zoezi hili pamoja na elimu bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, napenda nizungumze mambo machache kuhusu changamoto za wanafunzi. Zipo changamoto nyingi lakini kuna mambo ya msingi ambayo mwanafunzi akiyapata, akili yake itatulia na atasoma vizuri. Kuna suala la Bima ya Afya, mikopo na hosteli; na mambo mengine nitakuletea kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bima ya Afya bado ni tatizo. Wanafunzi wanaingia mwaka wa kwanza kwa mfano, toka wanavyoingia mwezi wa Kumi unakuta mwanafunzi hapati kabisa Bima ya Afya, sasa tatizo ni nini? Nakumbuka nilizungumza hili tatizo wakati nikiwa kwenye Kamati ya Huduma, bado tatizo linaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri ashughulikie kwa sababu vijana hawa wanahitaji kupata afya ili waweze kusoma. Pia wakati mwingine mwanafunzi anapata Bima ya Afya mwezi wa Tano, mwezi wa Saba ina-expire, wanaomba expiring date iendane na ile date of issue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mikopo; mikopo inakwenda vizuri lakini bado kuna changamoto. Wamepongeza sana ule mtindo wa fingerprints, wanapenda utumike huo, lakini kuna wakati vijana wanasaini mkopo wanasema fedha zimekuja, lakini wanaweza wakakaa zaidi ya hata ya mwezi fedha hizi hazijaja, kwa hiyo kuna shida. Hata hivyo, wameipongeza sana Bodi ya Mikopo Taifa kwa jinsi wanavyoshirikiana na wanafunzi hawa, tatizo bado liko kwenye kanda. Kwa hiyo kwenye kanda muweze kuelekeza nguvu waweze kuwasaidia hawa vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hostels ni muhimu sana kwa vijana wetu. Wapo wanafunzi wanabakwa usiku, mfano hapa Muslim University, Mipango, wasichana wawili wamebakwa wakati wanatoka shule wanakwenda majumbani kwao, kwa hiyo hostels fedha zilizotolewa tunaomba zitolewe zote ili ziweze zikajenge kule Mzumbe, SUA, Dar es Salaam kama tunavyoona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la rushwa na maadili; wakati wa orientation nimwombe Mheshimiwa Waziri ajitahidi kwamba orientation vijana hawa wapewe namna ya maadili. Kwa mfano suala la rushwa ya ngono, suala hili mara nyingi wanaelekezwa Walimu wa kiume tu, lakini kwa jinsi nilivyokaa na wanafunzi na walimu hii ina-apply kotekote, wapo wanafunzi wa kike ambao wanawa-seduce Walimu wa kiume na meseji nimeziona. Kwa hiyo tunaomba rushwa ya ngono, hasa kwa Wahadhiri vijana ndio wanatuhumiwa zaidi, lakini hawa Seniors Professors wako vizuri, vijana wanawapongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la fieldwork; kwa mfano upande wa mining, petroleum na gesi ni shida, vijana wanapelekwa kwenye vikampuni vidogovidogo. Sasa kama tunataka tutumie wataalam wazawa, inabidi yale makampuni makubwa yasaidie kuwapokea hawa vijana wetu kwenye suala la field kwa sababu field nayo ni changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipitisha humu ndani asilimia 15 kwa ajili ya kulipa mkopo. Kwa kweli asilimia 15 hii bado ni kubwa, kama inawezekana waweze ku-review, kwa sababu huyu kijana anapoanza kazi, kwanza tayari anatoka kwenye familia ya kipato cha chini, halafu bado unambebesha tena asilimia kumi ya penati akichelewa kulipa; bado alipe asilimia 15, anatakiwa alipe asilimia 30 ya tax, sijui mambo ya bima na kadhalika, please, tunaomba waangalie, asilimia 15 ni kubwa sana. Mbona mikopo ya vijana kule halmashauri tumeondoa riba; kwa nini tusiondoe na huku kwa vijana wetu ili tuweze kuwasaidia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Wahadhiri, vyuo vikuu tunategemea sana Wahadhiri wetu wafanye kazi vizuri, lakini kuna hii, Mheshimiwa Waziri anajua, yeye ni profesa ametoka kule, suala la harmonized scheme. Kule mwanzoni watu waliajiriwa wakiwa na GPA ya 3.5, wengine 3.8, baada ya harmonized scheme wanatakiwa wote kuwa na 3.8, sasa hii inaleta changamoto kwa ambao waliajiriwa kwenye 3.5, ni vizuri wakaanzia pale walipoanza hii sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kuna suala la stahiki za Walimu kama walivyoongea Wabunge wengine. Walimu wanadai arrears zao, wanadai responsibility allowances, housing allowances, for so many years; wanasubiri nini jamani? Hawa nao ni binadamu wana majukumu yao, lakini wasije wakashawishika sasa wakaanza underground migomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, nikiangalia kwenye bajeti yetu hii universities maana yake kuwe na research and development; fedha hazipo. Serikali wanatoa kiasi kidogo, sasa hili Taifa tutaendeleaje? Kwa mfano, sasa hivi kuna uhaba wa ajira, Walimu ni wachache, hawaaajiri lakini bado researches zenyewe hata promotion haziji. Unajua hadhi ya chuo kikuu lazima watu wapande wafikie ngazi fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano sasa hivi kuna hili suala la Walimu ambao ni Senior Professors kustaafu kwenye age ya 65. Sasa wale wengine sasa hivi mnasema Maprofesa waliostaafu wasipewe hata mikataba labda kama chuo kiwagharamie. Vyuo hawana fedha za kutosha, lakini tukumbuke kwamba hawa Maprofesa ambao tunawaacha, nafikiri ni kwa Tanzania tu, wangefikiria, kama suala ni gratuity wangefanya kama India, India profesa anastaafu kwenye age ya 65 lakini wanalipwa mishahara gratuity haipo. Kwa nini wasikae chini waongee? Kwa sababu vyuo vyetu vitakosa credibility, hili wanaliona, tutakwenda kwenye bomu kama la sekondari; shule za Serikali hazi-perform, private zina-perform.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Serikali imetumia fedha nyingi kumuandaa Profesa, unajua kumwandaa profesa sio kazi ngumu, wanawaacha watachukuliwa huko na private sector, hata nchi za nje, baadaye tutakosa sifa tutaanza kuagiza ma-TX. Sasa kumlipa TX cha bure ni gharama, TX umsomeshee mtoto, umlipe kwa dola na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, please, nimwombe Mheshimiwa Waziri hebu wakae walifikirie…

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri. Mheshimiwa Mama Salma Kikwete.

MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA – MAKAMU MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MASUALA YA UKIMWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuhitimisha hoja yangu.

Kwanza kabisa napenda kuwashukuru Wabunge wote kwa michango yenu mizuri ambayo imelenga kuboresha katika vita hii ya kupambana na masuala ya UKIMWI, dawa ya kulevya lakini pia na kifua kikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nawapongeza sana Mawaziri kwa kufafanua. Suala la UKIMWI ni suala mtambuka kwa hiyo, liko katika sekta zote, kwa hiyo basi Wizara kama ya Michezo ikiboresha mambo yake Wizara ya Elimu ikiboresha mambo yake, hata changamoto zile ambazo zinasababisha watu kupata UKIMWI zinapungua. Kwa hiyo, tunawashukuru Mawaziri kwa juhudi zenu katika kuboresha mambo ya kijamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani za pekee zimwendee Mheshimiwa Waziri, Ummy Mwalimu kwa kutufafanulia kutupatia data ya hivi karibuni ya kuhusu suala la 90, 90 ambalo watu wengi wamezungumzia. Kwa hiyo, tunashukuru, lakini tunaomba juhudi hizi ziendelee kufanyika ili kwa sababu mwaka huu 2020 ndio mwaka ambao tunatakiwa tufikie 90, 90 zote tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Wabunge ambao wamechangia hoja walikuwa sita, kwa sababu ni wachache naomba kuwataja majina; Mheshimiwa Susan Lyimo, Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mheshimiwa Mboni Mhita, Mheshimiwa Amina Mollel, Mheshimiwa Edward Mwalongo na Mheshimiwa Sikudhani Chikambo, lakini na Waheshimiwa wengine wakati wanaanza pia waliipongeza Kamati yetu kwa kazi nzuri ambayo tumeifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, michango ya Wabunge ambao wameonesha hoja zao mingi kabisa ilikuwa imejikita kwenye maeneo yafuatayo; suala la 90-90-90 limezungumzwa, suala la kuhakikisha kwamba Serikali inatafuta vyanzo vya uhakika ambayo Kamati pia imezungumza, imejitokeza. Pia imejitokeza wamechangia kwamba watu waweze kupima ili waweze kutumia dawa ili tuweze kufikia 90-90; lakini pia jambo lingine lilizongumzwa na wachangiaji ni kuharakisha utekelezaji wa Sheria ya Mtoto ya miaka 15 ambayo inamruhusu sasa kupima bila ridhaa ya mzazi ili hasa tuweze kufikia 90 ya kwanza ile ambayo ni muhimu sana kwa 90 pili na ya tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia mchango mwingine ulijikita kwamba elimu zaidi sasa iendelee kutolewa ili watu waelewe zaidi masuala ya UKIMWI, TB na madawa ya kulevya. Pia kuna mchangiaji mwingine ambaye amesema basi Serikali iangalie namna ya kutoa msamaha wa kodi kwa NGOs zinazojishughulisha na masuala ya UKIMWI, TB na madawa ya kulevya ingawa wakati tumekutana na Mheshimiwa Waziri wa Fedha alitufafanulia kuhusu jambo hili. Zipo NGOs kwa kufuata utaratibu maalum wanaweza wakapata huo msamaha wa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema Waheshimiwa wengine Wajumbe wamepongeza Kamati kwa kazi nzuri. Kwa hiyo, hakukuwa na mambo mengi sana ambayo yamejitokeza, sana sana wachangiaji wengi wamepongeza Kamati kwa kazi nzuri na issues ambazo zimetokea wamezizungumza zote ziko kwenye Kamati. Niwashukuru kwamba na wenyewe wameona na wanapongeza juhudi ya Serikali katika kupambana na suala hili la UKIMWI, madawa ya kulevya pamoja na TB. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niseme tu kwa kuhitimisha kwamba magonjwa haya kwa kweli ni hatari hasa upande wa UKIMWI kwa sababu hata kama Serikali itaweka trilioni za fedha kama hatutabadili tabia zetu bado ugonjwa huu hatutaweza kufikia lengo la 2030. Kwa hiyo tubadili tabia tuweze kulindana ili kuweza kufanikisha kutatua changamoto hii ambayo inatukumba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nashukuru sana kwa kunipa nafasi, baada ya kusema haya nahitimisha hoja yangu na naomba kutoa hoja. Ahsante. (Makofi)

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.