Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Cecil David Mwambe (1 total)

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba Serikali ya Tanzania imepitia Awamu Sita za uongozi; Awamu ya Kwanza ilijikita kwenye kujenga viwanda kwa ajili ya kuboresha ajira na uzalishaji, Awamu ya Tatu iliamua kubinafsisha viwanda hivi ili kuviboresha zaidi pamoja na kuongeza ajira, Awamu ya Tano ilikuja tena na Sera ya Ujenzi wa Viwanda ili kuongeza ajira pamoja na uzalishaji.

Swali langu; viwanda vilivyobinafsishwa kwenye Awamu ya Tatu vingi havifanyi kazi iliyokusudiwa, kwa mfano viwanda vya korosho Mkoa wa Mtwara, Lindi pamoja na Ruvuma. Nini msimamo wa Serikali wa Awamu ya Sita kuhusu viwanda vilivyobinafsishwa ambavyo havifayi kazi iliyokusudiwa? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba uchumi wa nchi yetu hutegemea nyanja nyingi ikiwemo na ujenzi wa viwanda ambavyo vina faida pana kwa Watanzania na mifano yote uliyoieleza kutoka Awamu ya Kwanza mpaka ya Tatu. Awamu ya Tatu ya Serikali yetu ililenga kutoa fursa kwa Sekta Binafsi kuhakikisha kwamba nazo zinaingia kwenye mchakato wa uchumi kwa kushika viwanda na kuviendeleza. Lakini nasikitika kwamba baadhi ya waliopewa viwanda hivyo hawakufanya vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini Serikali imefanya ni kuchukua viwanda vyote ambavyo havikufanya vizuri na tuliunda Tume iliyoongozwa na Msajili wa Hazina pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kufanya mapitio viwanda vyote vile ambavyo vilibinafsishwa na havifanyi kazi ikiwemo na viwanda vya korosho. Na kwa bahati nzuri mimi ni mdau wa korosho na natambua viwanda vyetu kule vingi hata vilivyopo Mkoani Pwani na Tanga wameshindwa kuviendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tulichofanya, tumechukua viwanda vyote na sasa vinafanyiwa uchambuzi na Serikali na timu iliyoongozwa na Msajili wa Hazina baadaye tupeleke kwenye Baraza la Mawaziri. Malengo yetu ni kutoa viwanda hivyo kwa watu ambao wana uwezo sasa kwa sababu Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan anasisitiza pia kwamba Sekta Binafsi lazima iwe karibu na Serikali ili kuweza kupanua wigo wa uchumi kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, baadaye tukipata wale ambao wana nia ya kuendesha tutawapa kwa masharti ambayo tutayaweka ili kuendeleza ule mkakati wetu wa uchumi wa viwanda hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie tu mheshimiwa Mbunge kwamba viwanda hivi ambavyo havifanyi kazi tayari vimesharatibiwa na vitatolewa kwa watu ambao wenye uwezo. Kwa hiyo, niwakaribishe Watazania wenye nia ya kuwekeza kwenye viwanda kuwa tayari kupokea baada ya Baraza la Mawaziri kufanya maamuzi ili waweze kuviendesha viwanda hivyo kwa ufanisi mkubwa zaidi kuliko ilivyo hivi sasa, ahsante sana. (Makofi)