Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika (21 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. CAPT. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kusema na kwa sababu katika Bunge hili ni mara yangu ya kwanza kuzungumza. Nataka niwashukuru wapiga kura wangu wa Jimbo la Newala Mjini kwa kunirejesha tena katika jengo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo mengi ya kusema kabla sijaenda mbali. Nikiwa ndiye Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini wa Klabu ya Yanga nataka kuipongeza klabu yangu ya Yanga kwa kuchukua ubingwa. Vijana wetu tunawapongeza, mmefanya yale tuliyowatuma mfanye, tunataka mfanye hivyo na nchi za nje pia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mimi nataka nichukue nafasi hii kuwapongeza maraisi waliotokana na Chama changu kwa kushinda uchaguzi. Tupo awamu ya tano ya maraisi, na faraja niliyonayo kwamba wote waliopokezana vijiti wametoka Chama cha Mapinduzi.
Nampongeza Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kushinda, nampongeza Mheshimiwa Makamu wa Rais, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, naipongeza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mheshimiwa Makamu wa Pili wa Rais, Mabaraza ya Mawaziri yote ya Muungano na lile la Baraza la Mapinduzi Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuna kazi moja tu ya kutekeleza Ilani ya Uchaguzi, pamoja na Waheshimiwa Mawaziri chapeni kazi. Ukimsikia mtu anakuambia mnakwenda kasi muulize nilipoapishwa niliambiwa niende speed gani? Kwa hiyo, mimi nataka kupongeza sana. Lakini wanasema mnyonge mnyongeni haki yake mpeni. (Makofi)
Ndugu zangu uongozi wa nchi ni kupokezana. Kabla ya Magufuli tulikuwa na Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, kafanya mambo mengi nchi hii. Mimi nataka niwape mfano ambao ni my personal experience.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilimaliza shule form four mwaka1967 wengi mlikuwa hamjazaliwa. Shule inaitwa St. Joseph College Chidya, nikapelekwa kwenda Ilboru, kwa sababu ya matatizo ya mawasiliano ya Mtwara na Arusha mimi nilikuwa natembea wiki nzima kwa gari katika barabara ya vumbi kutoka Newala, Nachingwea, Tunduru, Songea, Njombe, Iringa, Morogoro nikifika Chalinze napanda basi kwenda Arusha; wiki nzima niko njiani, hatukuwa na barabara ya lami. Akaja Mzee Mwinyi akatuanzishia daraja, Mzee Mkapa akatujengea daraja, Jakaya akatuwekea lami. Leo unatoka Newala kwa gari saa nane mchana na saa mbili jioni upo Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amefanya kazi nzuri, ametuwekea sekondari kila kata, amejenga barabara za lami nchi hii, kama ilikuwa ni kushindana ndiye anayeongoza kwa kujenga barabara za lami nyingi kuliko waliomtangulia. Kigoma mlikuwa mnalalamika tupo gizani, ameondoa tatizo la umeme, amewawekea daraja mto Malagarasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwanza tunampongeza Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, ameiongoza nchi salama miaka kumi amemaliza, kijiti amemkabidhi Mheshimiwa John Pombe Magufuli, sasa sikilizeni kazi ya Magufuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya miezi sita tu vijana wanasoma bure toka fstandard one mpaka form four, ndani ya miezi tu. Ndani ya miezi sita amesema ile Mahakama ya Ufisadi mliyokuwa mnaidai tarehe 01 mwezi Julai inaanza. Miezi sita bado…
(Hapa baadhi Wabunge walizungumza bila kutumia vipaza sauti)
Mtu mzima naongea mambo ya kuzomea zomea wakati hujaruhusiwa, mtu mzima anaongea. Mimi nilidhani mnawafanyia vijana wenzenu hata mimi size ya mzee wenu? (Makofi)
MKUCHIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hii disturbance iliyotokea utaniongezea muda. (Makofi/Kicheko)
Kwa hiyo nasema nchi ipo salama. Ametoka Rais wa CCM amemkabidhi kijiti Rais wa CCM, ilani ya uchaguzi iliyokuwa inatekelezwa sasa Mheshimiwa John Pombe Magufuli amechukua pale alipoacha Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, ndiyo maana nchi ipo shwari, haijashikwa na watu wababaishaji, imeshikwa na watu makini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya kusema hayo niseme mengine. Kwanza nataka niombe sana Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli ana nia nzuri na nchi hii, Mawaziri wake wana nia nzuri na nchi hii, hebu tuwape ushirikiano ili Tanzania pawe mahala pazuri pa kuishi. Mbona kila nchi nje huko wanatupongeza? Wanawashangaeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya kusema hayo nataka kwenda kwenye barabara. Nataka niishukuru Serikali yangu ya CCM Serikali sikivu, watu wa Mtwara tumeomba barabara ya lami kutoka Mtwara – Tandahimba – Newala – Masasi. Hotuba ya Waziri inasema bajeti ya mwaka huu kuanzia tarehe 1 Julai, 2016 barabara inajengwa. Naomba watu wa Tandahimba, Newala, Masasi, Mtwara, kazi mliyotutuma tumeifanya majibu ya Serikali ndio hayo, barabara itajengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili barabara ya mkoa. Mheshimiwa Waziri Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Mtwara tumeomba barabara ya mkoa kutoka Newala – Nyambe – Ndanda ichukuliwe na mkoa kwa sababu, watu wa Tandahimba na Newala Hospitali yetu ya Rufaa ni Ndanda. Tunaomba ombi hilo lichukuliwe barabara iwe ya mkoa ili iweze kutengenezwa vizuri kwa sababu, Halmashauri zetu uwezo umekuwa mdogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Newala tulikuwa na uwanja wa ndege ambao umetumika sana wakati wa vita vya Msumbiji. Bahati mbaya nyumba zimejengwa karibu sana mpaka uwanja wa ndege ule umefutwa, lakini Halmashauri imeomba ipewe barua rasmi ya kuufuta uwanja wa ndege wa Newala, hilo jambo halijafanyika, tunaomba lifanyike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, Wilaya tumetafuta eneo la kuweka uwanja wa ndege, Waziri uliwatuma wataalam kuja kuona, wametuambia shughuli gani tufanye.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba suala la ujenzi wa uwanja wa ndege Newala, utakapokuwa unajibu, watu waliozoea kuwa na uwanja wa ndege tangu enzi ya mkoloni sasa inapokuwa hatuna uwanja wa ndege tumerudi nyuma. Tutapenda kusikia kauli ya Serikali kuhusu lini mnaanza kujenga uwanja wa ndege wa Newala, lakini kwa hatua za awali tunaomba wale watu wafidiwe eneo lile mlichukue. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Newala tuko mpakani na Mto Ruvuma; nimeona hapa hotuba kivuko hapa, kivuko hapa, sisi tuna mawasiliano ya karibu sana na Msumbiji. Kuna daraja kule la Umoja, kuna daraja la Kilambo, lakini Tandahimba na Newala pale tuna vivuko vingi na nafikiri ndio tunaingiliana zaidi na watu wa Msumbiji kwa sababu ya kupakana, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri, Wizara iangalie uwezekano wa kutuwekea kivuko katika Mto Ruvuma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, iko barabara inaitwa barabara ya Ulinzi, hii ni barabara inatoka Mtwara inaambaa ambaa kandokando ya Mto Ruvuma mpaka Tunduru mpaka mkoa wa Ruvuma. Barabara hii haijatengenezwa miaka yote na Serikali kuu, muda mrefu mmeaicha kuitengeneza, tunapata tabu kusomba korosho kwa sababu ya hali ya barabara na korosho za Mtwara nyingi zinatoka katika bonde la Ruvuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, nilikuletea barua, bado uko mgeni Wizarani kwamba, vijiji vya bonde la Ruvuma Wilaya yangu ya Newala, hawana mawasiliano ya simu. Walikuwa wanatumia simu za Msumbiji ambazo dakika moja tu shilingi 1,000, lakini haraka haraka ulituma watu wako, watu wa Halotel wakaja, bonde la Ruvuma leo Halotel ni Halotel kweli kweli. Tatizo lile la watu wa Newala, watu wa Tandahimba kutumia simu za Msumbiji umetuondolea tuko ndani ya Halotel ndani ya nchi yetu. Mheshimiwa Waziri, mimi nataka nikushukuru sana kwa uharaka wako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nakushukuru, lakini kwa kumalizia uwanja wa ndege wa Mtwara uwe uwanja wa Kimataifa wa Mtwara. Ninakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. KAPT. MST. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Napenda nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuteuliwa kuongoza Wizara hii, lakini nataka nikupe pole kwa kazi ngumu iliyoko mbele yako, kati ya wewe na wapiga kura wangu, wanaotegemea Mradi wa Maji Makonde, ambao upatikanaji wa maji badala ya kupanda umeporomoka. Tunapata maji asilimia 30 ukilinganisha na vijiji vingine au Wilaya zingine ambako wameshafika asilimia 65 vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea Waziri hoja yangu ni kwamba wala hatutaki Tandahimba, Newala Mtwara kunakofika huu mradi, hatutaki hela za kuendesha mradi, tunataka hela za kukarabati mradi ili kuongeza uzalishaji wa maji. Mchango wa wananchi wanaotegemea mradi huu kwa Serikali kila mwezi ni mdogo sana, kwa sababu maji mnayotuuzia ni kidogo sana, hatuna tatizo la kuchangia maji kwa sababu tangu tulivyoaanza Makonde Water Corperation tulikuwa tunanunua maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ujumbe wangu siyo kupitisha mafungu ya kuwezesha uendeshaji wa Mradi wa Maji Makonde, hoja leo hapa utakapokuwa unamalizia kesho kutwa, ueleze nini Wizara yako inafanya kuongeza uzalishaji maji kwa Mradi wa Maji Makonde. Mheshimiwa Waziri wewe umefika kule lakini nataka kukuomba, Naibu Waziri alikuja juzi wakati mvua inanyesha, watu wa Tandahimba, Newala ni hodari kwa kuvuna maji, kila nyumba ya bati utakayoiona tunachimba kisima, tunavuna maji ya mvua, mimi naishi kijiji kwangu, sina maji ya bomba katika nyumba yangu, nina visima viwili, napata maji ya shower na ya kunywa kwa sababu tunachimba visima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa Tandahimba na Newala kama wangelitegemea tu maji ya bomba ya Serikali hali yetu ya maisha ingekuwa ngumu sana. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri ninachoomba hapa siyo utueleze unafanya nini katika administration uendeshaji wa Mradi wa Maji Makonde, aaah aah! Utakapokuwa una- wind up utoe maelezo nini Wizara yako inafanya kuongeza uzalishaji wa maji katika Mradi wa Maji Makonde. Hiyo ndiyo hoja yangu, umri huu siyo wa kutoa shilingi, lakini kama hutatufikisha huko, kuna vijana wengine humu ndani wanategemea mradi huo huo mimi nitakaa pembeni huku nawapigia kwa chini chini (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Maji Makonde, Tatizo la maji Newala, Tandahimba ni kubwa kwa sababu ya jiografia, ile inaitwa Makonde plateau, niliposoma jiografia niliambiwa a plateau is arised flat peace of land. Plateau ni kitu gani, ni eneo ambalo limeinuka, na juu kuko flat ndivyo ilivyo uwanda wa Makonde ukija kwetu Tandahimba na Newala, ukienda Masasi, Mto Ruvuma, Lindi, Mtwara unateremka, ndiyo maana katika eneo la kwetu hatuna agenda visima vifupi haipo. The water table is so below unaweza ukachimba hata maili ngapi sijui, siku hizi mnatumia kilometa, unaweza ukachimba sijui kilomita ngapi hujapata maji, hatuna visima vifupi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia hapa the oldest scheme ya maji ambayo inaendeshwa na Taifa ni Mradi wa Maji Makonde, lakini naona tumepewa shilingi bilioni mbili. Shilingi bilioni mbili upeleke maji Tandahimba yaende mpaka Mtwara, mradi mwingine wa Kitaifa three hundred thirty thousand Euro, mradi mwingine twenty thousand billion, mradi mwingine three point; Mradi wa Maji Makonde shilingi bilioni mbili, Waziri naomba hili jambo ulitazame.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo sitaki kwenda katika historia, watu wa Newala - Tandahimba baada ya kuona shida zetu za maji ni kubwa, enzi ya mkoloni 1953 tulianzisha kampuni iliyokuwa inaitwa Makonde Water Corporation, kwa wazee waliokuwepo hisa ilikuwa shilingi 20 kampuni ikaenda kukopa hela Uingereza ikaanzisha Mradi wa Maji Makonde na mwaka 1954 mradi ukafunguliwa kwa sababu palikuwa na cost sharing kila mwaka tulikuwa tunapeleka maji vijiji vipya, maji yakawa yanapatikana bila matitizo every domestic point.
Baada ya mradi kuchukuliwa na Serikali kusema sasa hapana, tuachieni tunaendesha sisi tumerudi nyuma. Nimekaa Bungeni hii term ya tatu, nilipoingia upatikanaji wa maji Newala ulikuwa 22 percent miaka yangu kumi ya kufurukuta pamoja na uzito niliokuwa nao tumeongeza asilimia nane tu. Kama miaka kumi asilimia nane mpaka tufike hiyo asilimia 65 itatuchukua miaka mingapi? (Makofi)
Mheshimiwa Waziri ninachotaka kusema Mradi wa Maji Makonde una matatizo makubwa yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo hayo ni pamoja na uchakavu wa mitambo, mabomba yale enzi ya mkoloni hayakuwa plastic yalikuwa ni ya chuma yameoza yametoboka kwa hiyo maji yanayopotea njiani ni mengi. Hatuna pampu za kutosha, wataalam hawatoshi, vituo vichache vya kugawia maji, kwa ujumla uzalishaji mdogo wa maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri utakapokuwa unajibu narudia tena ueleze mwaka huu Serikali inafanya nini kuongeza uzalishaji wa maji Makonde, nakuomba uje kiangazi, Waziri wako alikuja wakati wa masika hakuona shida ya watu, wakati wa masika ndoo moja ya maji shilingi 1,000!
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi mingine ndugu yangu pale Mheshimiwa Bwanausi ameelezea, mradi wa maji Chiwambo ulikuwa unafika mpaka Newala hauji tena, Mradi wa Maji wa Luchemo tulipata mafuriko mwaka 1990 mashine zile zikasombwa na maji tangu 1990 mpaka leo hakuna replacement. Mheshimiwa Waziri naomba sana fufueni Mradi wa Luchemo tuunganisheni watu wa Newala na Mradi wa Chiwambo kwa ndugu yangu Mheshimiwa Bwanausi na ninashukuru ameuzungumzia hapa, naomba sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kwamba tunapata taabu Viongozi, mradi wa maji wa Kitangari – Mitema, Mji mdogo wa Kitangari upo kilomita tatu kutoka pale, hawapati maji. Maji yale ya Mitema yanasukumwa yanafika mpaka Tandahimba, hapa kwenye source ya maji hawapati maji.
Mimi mnanipa taabu sana maana inabidi niwabembeleze wapiga kura wangu, wanataka wapige shoka maji yale ili tukose wote, nawaambia hapana subirini Serikali inachukua hatua, sasa mwisho nitaitwa muongo, hivi umri huu na mvi hizi niitwe muongo Mheshimiwa Waziri unafurahi? Hivyo, tuaomba tatizo la maji la Mji Mdogo wa Kitangari lishughulikiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo sugu ambalo watumishi wa maji Newala hawataki kusikia. Tumepitisha maazimio kwenye Halmashauri, marufuku kupeleka maji katika visima vya watu binafsi, palekeni maji katika domestic point za public pale ambapo kila mmoja anapata maji. Maafisa wako wanachofanya wanapeleka maji katika nyumba za watu binafsi, wanawajazia maji baadae wale wanawauzia wananchi maji ndoo shilingi elfu moja, ukiwaambia kwa nini hampeleki katika domestic point ambayo watu wote tunapata pale hawana majibu! Jawabu nini corruption. Hebu Waziri tamka kesho kutwa utakapo wind up na uwaagize watumishi wa maji Newala kwamba….
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja nakutakia kila la kheri mdogo wangu unijibu vizuri kesho kutwa. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. KEPT. MST. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nipate kuchangia kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Newala Mjini. Mimi nataka kutangulia kusema naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka nichukue nafasi hii kuwapongeza vijana wangu wa Young Africans Sports Club kwa kuchukua ubingwa wa nchi hii kwa mara ya tatu, kama nilivyowaagiza vijana, nataka mje Dodoma, mcheze mpira hapa Dodoma lakini mje na kikombe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka pia niwapongeze vijana wetu wa Serengeti Boys kwa kazi nzuri waliyoifanya jana kuifunga Angola. Nataka niwashukuru Watanzania wote waliochangia Serengeti Boys kufika mpaka pale na mimi nina imani watafika mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mkulima wa korosho, kwa hiyo nitazungumza masuala ya korosho. Kwanza, nataka nichukue nafasi hii kuwapongeza sana wakulima wote wa korosho katika nchi hii kwa sababu mwaka huu zao…

T A A R I F A . . .

MHE. KEPT. MST. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa hiyo nimeipokea na ninawaagiza vijana wa Yanga wakashinde mechi iliyobaki ya Mbao ili mjadala wa mezani usituhusu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nimesema nawapongeza wakulima wa korosho nchi nzima, mwaka huu limekuwa zao la kwanza kwa kuingiza mapato mengi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, leo mimi nina furaha sana, hakuna mjadala wa Wizara ya Kilimo ninaouchangia kwa raha kama leo kuliko mwaka wa jana. Kuna sehemu moja tu sijaridhika na nitawaambia, lakini nataka nianze kuipongeza Serikali kwa kutufanyia yafuatayo wakulima wa korosho. Kwanza Bodi imeundwa upya, juzi tulikuwa na mkutano wa wadau, ulikuwa mzuri, nawapongeza, hatujawahi kuwa na mkutano wa wadau mzuri kama wa mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka nikupongeze ndugu yangu Waziri kwa kuvunja ule uongozi wa Mfuko wa Uendelezaji wa Zao la Korosho, pale palikuwa pananuka rushwa. Watu waling’ang’ania pale, kila mwaka ni hao hao, ukitaka uwabadili haiwezekani, walikuwa wanafanyaje, wanajua wao. Na tumeona matunda sasa kwamba ule mfuko umekuja kwenye bodi mwaka huu, nitaeleza baadaye matunda yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza tena Serikali, juzi mmetutangazia, na ninataka wakulima wote wa korosho Mtwara, Mkinga, Pwani, Lindi mjue kwamba Serikali yenu juzi imetutangazia mwaka huu tutagaiwa sulphur bure, hiyo ndiyo neema ya Serikali ya Awamu ya Tano, tutagawiwa magunia bure, Mungu akupe nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nataka kuchukua nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kuondoa kero, mimi sitaki kurudia, lakini nataka kutaja zinazonihusu mimi mtu wa korosho. Kero ya unyaufu, mtunza ghala, task force, usafirishaji, ushuru wa chama kikuu; ninaiomba tu Serikali mkishafuta haya mhakikishe kwamba mikoani kule inatekelezwa kama mlivyoagiza. Kwa sababu msimu wa mwaka jana kuna mikoa ilipindisha baadhi ya maagizo ambayo mliyatoa, watu kule wakatozwa unyaufu, wakatozwa task force. Mheshimiwa Waziri, mimi naomba maagizo yatekelezwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichukue nafasi hii kupongeza sana Mfumo wa Stakabadhi ya Mazao Ghalani. Sisi kule Mtwara, Lindi, tunasema Mfumo wa Stakabadhi ya Mazao Ghalani ndiyo mkombozi wetu. Tumepata bei nzuri ya korosho mwaka huu, kubwa sana. Na hii imetokana na ushindani, siku zote wananunua India peke yake, mwaka huu wamekuja Vietnam, ushindani ule ndio umetufanya tupate bei nzuri. Wapo watu wanasema wao ndio wameongeza bei ya korosho, kama wewe umeongeza bei ya korosho, je, nani ameongeza Lindi, nani ameongeza Mkinga?

Mheshimiwa Naibu Spika, korosho mwaka huu tumepata bei nzuri kwa sababu ya ushindani katika mtindo wetu wa stakabadhi ya mazao ghalani kwa sababu ya ujio wa watu wa Vietnam.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkitaka kujua Watanzania kwamba kweli mwaka huu tumenufaika na korosho, mwaka jana wakulima wa korosho tuligawana shilingi bilioni 203 tu basi, lakini msimu huu uliomalizika tumegawana bilioni mia nane na tisa, kutoka shilingi bilioni 203 mpaka shilingi bilioni 809, hii ni hatua kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nihame hapo niende kwenye ushirika; hapa ndipo niliposema, nimesema na kusema. Mheshimiwa Waziri ushirika una misingi yake, Rochdale Principles za Cooperative Unions. Rochdale Principles za Cooperative Unions zimekuwa ndizo zinazofuatwa na International Cooperative Alliance. Moja inasema democracy ndani ya vyama, Serikali ihakikishe kwenye ushirika kuna democracy. Sisi kule Mtwara tuna chama kinaitwa TANECU, kina vyama 55 Newala na 124 Tandahimba, jumla vyama 179, hawawezi kusimamia hawa, kama ingekuwa kompyuta unasema computer overload, ndivyo ilivyo TANECU, Newala, uongozi unashindwa kwenda chama kwa chama.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepeleka miaka mitatu iliyopita, wameomba vyama Newala kwa muhtasari, Tandahimba kwa muhtasari, tunaomba mkutano mkuu union tugawe chama hiki, Mrajisi akaandika barua akasema gaweni, Mrajisi aliyekuwepo amehudhuria mikutano yote, agizo lake la kusema gaweni halikujadiliwa hata siku moja. Naomba Serikali kwa madaraka ya Mrajisi gaweni TANECU kwa sababu ndiyo matakwa ya watu wa Tandahimba na Newala. Mwaka jana, mwaka huu Council ya Newala, Council za Tandahimba wameomba kugawa TANECU ili pawe na ufanisi. Ndugu yangu Mheshimiwa Waziri, mimi na wewe tunapatana kweli, tunakosana katika hili moja tu basi, hili ukilimaliza basi! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nilitaka kusema hayo, lakini neema ya hela iliyoingia mwaka huu Mtwara imesababisha watu wengine kujitokeza uhodari wa wizi hasa kule Masasi, wizi mkubwa kwenye vyama vya msingi, mmekagua mmekuta shilingi bilioni tatu zimeliwa mmewabana wamerudisha, sasa bado shilingi bilioni 1.4 hazijarudi. Mimi naiomba Serikali, viongozi na watendaji walioshirikiana na vyama vya ushirika kutuibia hela yetu ya korosho wote washughulikiwe na vyombo vya dola, wote, msibague, msishughulike na vingozi wa vyama vya msingi peke yake, tazameni nani alishirikiana nao na yeye aende akasimame mahakamani. Hapo ndipo watu wa Mtwara na Lindi tutafurahi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka niseme ushirika wa TANECU umeandikishwa kama ushirika wa mazao, lakini wananunua korosho peke yake. Naomba Waziri, Vyama vya Ushirika vinunue na mazao mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kwa ushirika, nasema moja ya misingi ya ushirika niliyosema (Rochdale Principles) inasema corporate social responsibility, chama kikitengeneza faida kirudishe kiasi cha hela ile kwenye jamii, watengeneze barabara, wasaidie shule, wasaidie hospitali, vitanda vya wagonjwa; TANECU tangu imetengenezwa faida miaka nenda rudi, tumewasema, juzi ndiyo wameanza kutoa mifuko kumi ya saruji kwa ajili ya sekondari. Hivi hela inayotengenezwa TANECU unatoa mifuko kumi, si aibu? Mbona mifuko kumi mimi naweza kuitoa hata ukiniamsha usingizini? Kwa hiyo, wasimamieni, waulizeni kuhusu corporate social responsibility wanafanya nini.

Sasa mimi nataka kurukia kwenye suala la mihogo. Mimi nimeshukuru Serikali yetu imesaini mkataba na China, sisi Mtwara ndio wakulima wakubwa wa mihogo, mwaka 1974 nchi hii ilipata njaa, wakati National Milling inanunua mihogo tumelisha mikao kumi, mihogo iliyokuwa imenunuliwa na National Milling Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mtwara tuko tayari kupeleka mihogo China, Mheshimiwa Waziri tuambie lini inahitajika, tumeacha kulima mihogo kibiashara (commercially) tunalima tu ya kula sisi wenyewe, tumefurahi kusikia neema hiyo ya China.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho, naona kengele kama inapiga, sisi kule pia tunalima soya, soya ile imesimama kwa sababu haina soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho, naomba ndugu yangu simamia vile viwanda viwili vya korosho Newala vifufuliwe, wale watu walionunua, kimoja kinafanya kazi kwa robo na kingine hakifanyi kazi kabisa. Ahadi ya Rais alipokuja Newala ilikuwa kwamba viwanda hivi tutavifufua ili wananchi wa Newala wapate ajira…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. KEPT. MST. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nampongeza sana mdogo wangu Waziri, ameanza vizuri aendelee vizuri pamoja na Naibu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hasa maeneo yanayohusu Wizara yangu ya Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Kamati ambayo tumefanya nayo kazi, Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, imetuongoza vizuri miaka miwili hii. Mwenzangu aliyenitangulia wameshirikiana naye vizuri na mimi nilipofika nimepata ushirikiano katika miezi hii minne ambayo nimefanya nao kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushukuru kwa pongezi zilizotolewa na Kamati kwa vyombo vitatu vinavyofanya kazi katika Wizara yangu, kwa maana ya TASAF, MKURABITA na Mfuko wa Rais wa Kujitegemea. Kamati inakubali kwamba wanafanya kazi nzuri, wanaomba tu ikiwezekana wawezeshwe ili waweze kufanya kazi nzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwa upande wa TASAF, kwamba tupo TASAF Awamu ya Tatu, utekelezaji tumefikia walengwa asilimia 70, bado walengwa asilimia 30. Tunafanya utafiti sasa kujiandaa kwa utekelezaji Awamu ya Pili ya TASAF ya Tatu na lengo la Serikali ni kuwafikia walengwa wote ili Watanzania wote wanaohitaji msaada wapate kusaidiwa na Mfuko wa TASAF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lilikuwepo swali hapa kuhusu ajira ya wataalam, ilizungumzwa wataalam katika afya, lakini kwa sababu Bunge hili hushughulika na ajira kwa watumishi wote, ningependa kusema yafuatayo kuhusu ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua kuwa zoezi la uhakiki wa watumishi limeleta upungufu wa watumishi wa kada mbalimbali ikiwemo watumishi wa kada ya ualimu na afya, Serikali imetoa vibali vya kuajiri watumishi 15,000. Hao 15,000 tumekwishwa waajiri katika hao 4,000 wako afya, 4,000 wako elimu na hasa elimu ya sekondari kwa walimu wa sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshatoa ikama iliyoidhinishwa kwa mwaka 2017/2018 ambapo jumla nafasi zilizokubaliwa 52,436 wanatarajiwa kuajiri, tulikuwa tunaziba pengo la wale ambao wametolewa kwa ajili ya vyeti fake, sasa tunataka kuingia katika mchakato wa ajira zile 52,000 ambazo zilikwishaidhinishwa na Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka niseme, nimesikia hapa ndani na baadhi yao wameniandikia vikaratasi, kwamba zipo Halmashauri zahanati imefungwa au kituo cha afya kimefungwa kwa kukosa muhudumu.

Mimi naomba endapo kuna mtu yeyote, Mbunge au mwananchi yeyote anayenisikia ambako katika Halmashauri yake zahanati imesimama kwa kukosa muhudumu nipewe taarifa, tutamuajiri mara moja ili huduma za afya ziweze kuendelea. Maeneo mengine tunaweza tukasubiri, lakini kwa afya ya binadamu hatuwezi tukaendelea kusubiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, limegusiwa hapa suala la utawala bora na mimi ni Waziri wa Utawala Bora. Nisingelipenda kubishana sana, lakini nataka niseme hivi, utawala bora maana yake nini? Utawala bora maana yake ni watu kuishi katika jamii kwa kufuatana kwa sheria na taratibu walizokubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Tanzania sheria na taratibu walizokubaliana zinatoka hapa katika Bunge, kwa hiyo mtu anayekwenda kinyume na yanatoka hapa katika Bunge huyo anakwenda kinyume na Utawala Bora na anapaswa ashughulikiwe kwa sababu anakwenda kinyume na sheria za nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nataka niseme, magazeti ya leo kama mmesoma Daily News wameandika, gazeti la Habari Leo wameandika, kiswahili wameandika lile la kiswahili Tanzania yang’ara katika utawala bora, tumeambiwa katika nchi za Afrika Mashariki, Tanzania ni ya kwanza; Rwanda wanatushinda katika fighting corruption wao wa kwanza, sisi wa pili, lakini ile utawala bora ikiunganishwa, akina Mpango mnasema uchumi shirikishi, Tanzania ni ya kwanza katika Jumuiya ya Afrika ya Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maneno hayo yanaungwa mkono na TWAWEZA, maneno hayo yanaungwa mkono na Transparent International, maneno hayo yanaungwa mkono na REPOA, maneno hayo yanaungwa na World Economic Forum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi naomba yale mambo yetu mengine si vizuri tukalumbana. Mimi sikuona mahala, nimefatilia na bahati kipindi hicho pia nilikuwa Waziri wa Utawala Bora, sikuona mahala aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arumeru katiwa hatiani na Mahakama ya nchi hii. Kwa hiyo, unavyosimama hapa ukasema kapewa promotion mtu ambaye ametenda kosa hili, hili, hili nchi hii chombo peke yake chenye mamlaka ya kutafasiri sheria ni Mahakama, hakuna mahala yule mtu ametiwa hatiani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengine ambayo yamezungumzwa hapa ni kuhusu bomoa bomoa. Siwezi kujibu yote, lakini nataka niseme tunataka kutengeneza reli standard gauge, tunataka kupeleka barabara iwafikie watu, nyumba yako ipo barabarani tuiache? Mimi nasema Serikali hii haina double standard, nyumba za watu binafsi zilizoko barabarani zimevunjwa, sasa hivi jengo la TANESCO mali ya Serikali linavunjwa. Linavunjwa kwa nini, kwa sababu liko barabarani. Hii Serikali haina double standard. Habari …
(Makofi)

T A A R I F A . . .

AZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, kwa jinsi nilivyobobea katika siasa sikusudii kubishana naye, nakusudia niendelee tu kujenga hoja niliyokuwa naijenga. Yeye hakai Arumeru, mambo ya Arumeru hayajui. Mwenyekiti Mao Tse Tung anasema no research, no right to speak, anajua hao Madiwani wameingiaje? Hivi mimi inanihusu nini hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka nimalizie katika hilo suala la utawala bora. Mmegusia katika habari ya kufungia magazeti, nataka niseme hivi, katika utawala wa nchi hii hakuna vacuum, Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 ilikuwa inampa Waziri kufungia magazeti, baadae tumebadilisha Sheria katika vyombo vya habari kuna committee inayoitwa Content Committee, wale wanafuatilia kama gazeti au redio au luninga imekwenda kinyume wanamshauri Waziri Kamati (Content Committee) wanamshauri Waziri kwamba hawa hapa wamekwenda kinyume na sheria za nchi, Waziri anachukua sheria, hatukurupuki tu hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ile Sheria ya Vyombo vya Habari tulikuja tukairekebisha, tukaipitisha hapa. Kwa hiyo mimi nataka niseme kwamba suala la good governance (utawala bora) ni kuishi kwa kuzingatia sheria za nchi ambazo tumekubaliana katika jamii. Inawezekana wewe ulitaka sheria iwe hivi, iwe hivi, bado hujawa na majority ya kutunga sheria, fuata wale walio wengi walivyotunga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, palikuwapo na hoja kwamba watu wanakaimu muda mrefu bila kudhibitishwa. Nataka kusema kwamba ulitolewa mwongozo unaosema kwamba kabla hujamkaimisha, kabla hujamfukuza, wasiliana na Utumishi, Utumishi watambue kule kukaimu kwako ili utakapokuwa unaomba kwamba yule adhibitishwe liwe lisiwe jambo jipya kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine watu wanakaimishwa bila Utumishi kuhusishwa, watu wengine wanafukuzwa hata bila Utumishi kupewa taarifa. Tunaomba tu kwamba taratibu tu zifuatwe na taratibu zikifuatwa sisi tukiletewa majina hata kama ni upekuzi tunasimamia na zoezi linaenda kwa jinsi ambavyo limekusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dada yangu pale Mollel kauliza maswali mawili ya msingi sana. Tunawafanyaje darasa la saba wale? Tunafanyaje wale ambao tumewafukuza kwa sababu ya vyeti fake? Niseme lile la vyeti fake na hilo la watu wa darasa la saba; Serikali imekaa na TUCTA (Chama Huru cha Wafanyakazi), ni mambo ambayo tumezungumza, tunaendelea kuzungumza nao, tumepeana muda ili jambo hili tuweze kulimaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka niseme lile la vyeti fake, Serikali ilishasema kwamba kama mtu wakati wa kutafuta ajira alipeleka vyeti fake na yeye akaingia mkataba na Serikali maana yake mkataba wake ule ni null and void. Maana mwajiri alimtaka apelike cheti ambacho ni sahihi, cheti ni halali. Yule ambaye aliyepeleka cheti fake maana yake mkataba nao ni fake. Swali linakuja je, unamu-award mtu ambaye ana cheti fake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, TUCTA wameiomba Serikali na Serikali imeshasema, kama ni kuwashitaki wale wangeshtakiwa na TAKUKURU, wangeweza kushtakiwa na Kanuni za Utumishi, Serikali imetoa msamaha. TUCTA wametuomba kwamba tunaomba Serikali iwe na jicho la huruma kwa hawa watu wa darasa la saba, kwa hawa watu wa vyeti fake na Serikali inalifanyia kazi jambo hilo, muda utakapofika Serikali itatangaza uamuzi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sijui nimebakiwa na dakika ngapi, maana yake mambo yapo mengi ambayo yalikuwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru, naounga mkono hoja ya Kamati tunazozijadili, ahsante sana.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. CAPT. GEORGE H. MKUCHIKA - MWENYEKITI KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi tena. Sitamaliza hiyo robo saa kwa sababu Kamati yangu wamechangia watu watatu; hapakuwa na maneno mengi sana. Nadhani hiyo ni kuonesha alama wanazoipa Kamati, nadhani zaidi ya asilimia 90 hawakuwa na mambo ya kusema. Mheshimiwa Mwenyekiti, Wajumbe wawili wamechangia humu ndani, Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete na Mheshimiwa Dkt. Semesi. Mheshimiwa Juma Othman Hija alichangia kwa maandishi. Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, yeye ametoa rai kwamba kila Mbunge ajiheshimu mwenyewe kwanza. Sisi tunakubaliana naye na ndiyo msimamo wa Kamati yangu kwamba kama hapa ndani kila mmoja atajiheshimu, nafikiri hata kazi ya Kamati hii itakuwa rahisi sana. (Makofi) Mheshimiwa Dkt. Semesi amependekeza Kamati iwe na Wajumbe 50 kwa 50. Nataka nimweleze kwamba Kamati hizi hapa ndani zinaundwa kulingana na uwiano wa Wabunge kwenye Vyama. Kamati zote zilizomo humu ndani kile Chama ambacho kina Wabunge wengi ndicho kina Wajumbe wengi. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Kamati zote zinategemea hiyo. Ukichambua hizi Kamati, ni yale yale ninayoyakemea kwamba kwa utaratibu wa humu ndani, kama mmoja anaongea, wewe unanyamaza. Nadhani ndiyo mnaona umuhimu wa Kamati yangu, kwamba wako watu ambao lazima tushughulike nao ili hapa ndani pawe shwari. (Kicheko/Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukitoka hapa, nenda kachambue Kamati yote, in reality, ratio iko 7:3 nenda Kamati zote. Kwa hiyo, siyo kwamba hii Kamati ya Maadili isan exception, hapana. Ndivyo ilivyo kwa muundo wa Kamati zote. La mwisho, niseme tu kwamba anayeunda hizi Kamati, sio Wajumbe wa Kamati, ni Mheshimiwa Spika. Mheshimiwa Mwenyekiti, watatu, ndugu yangu hapa, Mheshimiwa Juma Abdallah Juma, yeye amechangia kwa maandishi, anaipongeza kazi ya Kamati na anapendekeza kanuni ziangaliwe upya ili kuwabana wanaofanya fujo ndani ya Bunge. Ninachotaka kusema ni kwamba, Kamati ya Kanuni ndiyo inayotengeneza kanuni, sisi tunafanya kazi kwa kutumia kanuni zilizotengenezwa na Kamati ya Kanuni na kupitishwa na Bunge Zima. Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nimalizie tu kusema kwamba sisi kama Kamati ya Maadili, tunatoa rai na kama tulivyosema pale mwanzo, hapa ndani kuna maendeleo makubwa sana. Ukilinganisha vurugu zilizokuwepo mwanzoni wakati Bunge linaanza na tulivyo leo, yapo mabadiliko makubwa. Kwa mtu yeyote ambaye akili yake haina matatizo, anaelewa kwamba tumepiga hatua. Yule ambaye hataki kuelewa, mwache aendelee kutokutaka kuelewa kwa sababu ndiyo watu wengine walivyo, lakini hali ya hapa katika Bunge nadhani kwamba tumeanza kwenda vizuri. Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nimalizie... Mheshimiwa Mwenyekiti, si ndiyo haya haya ninayokemea? Mimi si ndiyo nimepewa nafasi hapa kusema? Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimalizie kwa kusema hivi, tukiwa hapa ndani, naomba tuendelee kuheshimiana, kuvumiliana, kuzingatia kanuni, kuheshimu kiti na nimalizie kusema tu kwamba ukizomea wakati mwingine wanasema, haujajenga hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka leo tuondoke wote na msemo huu ambao katufundisha Baba yetu Mwalimu Nyerere. Alitufundisha hivi, argue, don’t shout. Tuondoke na spirit hiyo, Baba yetu katufundisha, “argue don’t shout.” Kama mwenzio anaongea, kapewa nafasi, nawe ghafla bin vup, unabonyeza unasema „nini wewe?” “Mambo gani hayo?” You are shouting. Argue, don’t shout. Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba Bunge lako Tukufu likubali kuipokea taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge pamoja na mapendekezo yake ili yakubaliwe na kupitishwa na kuwa maazimio ya Bunge. Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. CAPT. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, barabara ya Newala -Kitangari – Mtama inahudumiwa na TANROADs. Hii barabara inaunganisha Mkoa wa Mtwara na Lindi, lakini ni barabara ya vumbi. Wananchi wa Newala wanaomba barabara hii ijengwe kwa kiwango cha lami, maana pia ndiyo njia kuu wanayotumia watu wa Newala kwenda Dare es Salaam na Dodoma. Tunashukuru kwa jitihada za Serikali maana sehemu korofi kama za Kitangari na mlima Kinolombedo zimejengwa kwa kiwango cha lami. Ni vizuri kuongeza kilomita zilizojengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu Uwanja mpya wa Ndege wa Newala. Baada ya eneo la Uwanja wa Ndege wa zamani kupima viwanja, Uongozi wa Wilaya umetenga eneo jipya la Uwanja wa Ndege. Wataalam wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege walitembelea Newala na kuelekeza ukubwa unaohitajika na mwelekeo wa Uwanja. Nilipouliza swali Bungeni, Mheshimiwa Waziri alinijibu kuwa Serikali italipa fidia eneo la uwanja, wakati inafanya mipango ya Ujenzi. Wananchi wa Newala wanaomba Serikali ilipe fidia eneo la Uwanja wa Ndege ambalo halina mazao mengi ya kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami toka Newala Mjini kuelekea Masasi palitengenezwa mfereji wa kutolea maji barabarani. Mfereji huu umeleta uharibifu mkubwa kwa kutengeneza korongo kubwa zinazotishia usalama wa nyumba za wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika katika Kijiji cha Mkunya, korongo kubwa lililosababishwa na mvua linahatarisha usalama wa nyumba za wananchi. Alipotembelea Wilaya ya Newala, Mheshimiwa Waziri Mbarawa alikagua eneo la korongo la Newala Mjini, akaahidi kutafuta fedha za kujenga makorongo hayo vizuri. Wananchi wa Newala tunakumbusha ahadi ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuanza kutoa maelezo yangu kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge letu kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge na kuhitimisha hoja za Makadirio ya Bajeti ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa mwaka wa fedha 2018/2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kwa mara nyingine tena kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais kwa maelekezo yake yanayoniwezesha kutekeleza majukumu ya kusimamia menejimenti ya utumishi wa umma na utawala bora, eneo ambalo ni mtambuka katika utawala wa nchi na utendeshaji wa shughuli za Serikali. Napenda pia kuwashukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kwa maelekezo na ushauri wao ambao unatuwezesha kumsaidia Mheshimiwa Rais kwa ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kukushukuru wewe binafsi pamoja na Mheshimiwa Spika, Wenyeviti wa Bunge, Katibu wa Bunge na uongozi wote wa Bunge kwa ushirikiano mkubwa mnaoipatia Ofisi yetu katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani zangu ziwaendee viongozi na wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa maoni na ushauri walioutoa ambao umesaidia katika utekelezaji wa majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo kwa awamu zilizotangulia, Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea kuheshimu Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na kutekeleza sera na mipango ya taifa kwa muda mrefu iliyobuniwa kuwaondolea wananchi umaskini na kuwaletea maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa sera, mikakati na mipango hii unahitajika watumishi wa umma wenye weledi, uadilifu, uchapakazi na umakini kwa kuwa utumishi wa umma ni nguzo muhimu katika maendeleo ya Taifa letu. Ikumbukwe kuwa kila taasisi ya umma imejengwa na watumishi wa umma, na bajeti zilizoombwa leo hapa zitakazopitishwa, wizara zote utekelezaji wake kwa kiwango kikubwa unategemea watumishi wa umma ambaye mimi ndio Waziri wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nia ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuendelea kuiboresha sekta ya utumishi wa umma, kuhimiza misingi ya weledi (professionalism), kuweka mifumo ya menejimenti inayowezesha watumishi kuwajibika na kuwa na maadili ili watoe huduma kwa wananchi na wadau wengine kwa kufanya kazi kwa ufanisi, bidii na kuzingatia matokeo na hivyo kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, utumishi wa umma lazima uongozwe na kusimamiwa ili kuhakikisha kuwa unaboreshwa kulingana na mahitaji ya wananchi bila kuathiri misingi yake. Ili kulinda misingi Serikali imekuwa ikifanya mabadiliko katika usimamizi wa utumishi wa umma mara kwa mara ili kuendana na misingi niliyoieleza hapo awali. Kama ilivyo kwa awamu zilizotangulia, Serikali ya Awamu ya Tano itaendelea kuuboresha utumishi wa umma ili uendelee kuwa na manufaa kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu kuanza kwa Serikali ya Awamu ya Tano, hatua mahususi za kusimamia sera na mifumo ya menejimenti, matumizi ya teknolojia na habari na mawasiliano, nidhamu, mapambano dhidi ya rushwa, uadilifu na uwajibikaji imeendelea kuchukuliwa. Tunaamini kuwa kwa kuzingatia mambo haya watumishi wa umma watafanya kazi kwa weledi na bidii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia Wizara yangu; Wabunge 74 wamechangia hotuba yangu kwa kuzungumza hapa ndani ya ukumbi wa Bunge na Wabunge 17 walichangia kwa maandishi. Wabunge hawa wakiongozwa na Mheshimiwa Jasson Rweikiza, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa na Makamu wake Mheshimiwa Mwanne Mchemba wametoa michango na ushauri ambao tutauzingatia wakati wa kutekeleza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyoona hii ni idadi kubwa ya Wabunge waliochangia, napenda kuwashukuru sana, muda ungetosha ningewataja mmoja mmoja, lakini kwa sababu ya muda naomba wanisamehe. Napenda kuwashukuru sana na kuwaahidi kuwa maelezo kwa kila hoja iliyotolewa yatapatikana kabla ya mkutano huu wa Bunge kumalizika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja katika Wizara yangu zilijikita katika maeneo mahusisi yafuatayo, yaani yale yaliyozungumza kama unataka kufanya majumuisho mengi yamegusia maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza upungufu wa watumishi hasa katika sekta ya afya na elimu ambayo imechangiwa na Wabunge 39, upandishwaji vyeo iliyozungumzwa na Wabunge wengi, watumishi kukaimu nafasi na madaraka kwa muda mrefu kama ilivyojitokeza kwenye maoni na ushauri wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, umuhimu wa kuboresha maslahi ya watumishi ambapo Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa imelitolea maoni na ushauri. Aidha Wabunge wawili nao wamelizungumzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia mapambano dhidi ya rushwa, masuala ya utawala bora ikiwemo wasiwasi na usalama wa wananchi wetu na shughuli za Idara ya Usalama wa Taifa, suala ambalo lilichangiwa na Wabunge 17 na leo nitalitolea ufafanuzi; vita dhidi ya umaskini kama lilivyojitokeza katika maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa na michango ya Wabunge waliochangia kuhusu shughuli za TASAF, MKURABITA na Mfuko wa Rais wa Kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba majina ya Waheshimiwa Wabunge wote kama nilivyosema yaingie kwenye hansard kwa kumbukumbu sahihi za shughuli za bajeti za Wizara yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza hapo awali, masuala haya ni sehemu kubwa ya ajenda ya Serikali ya Awamu ya Tano kama ilivyoelekezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi 2015/2020 na napenda kuchukua nafasi hii kuyazungumza kwa kifupi hasa kwa kuwa muda hautoshi kujibu hoja zote kama zilivyotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Nitajitahidi kujibu hoja kwa kadri muda utakavyoruhusu, na naomba nianze na suala la ajira katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na rasilimali ya kutosha na yenye weledi katika kutekeleza majukumu yake kulingana na vipaumbele vyake. Hata hivyo, ajira katika utumishi wa umma hutegemea uwezo wa bajeti ya Serikali, pale bajeti inaporuhusu Serikali imekuwa ikitoa nafasi za ajira. Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga nafasi za ajira 49,356 ikiwemo nafasi 16,000 za walimu wa shule za msingi na sekondari, nafasi 15,000 kada ya afya na kada nyingine za kilimo, uvuvi, mifugo, vyombo vya ulinzi, magereza, uhamiaji na nafasi 15,245 kwa ajili ya kada nyinginezo wakiwemo Watendaji wa Vijiji, Mitaa na Kata, Wahasibu, Wahadhiri wa Vyuo Vikuu, Maafisa Tarafa, Maafisa TEHAMA, Ugavi, Utawala na Utumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili lililochangiwa na Wabunge wengi ni lile la upandishwaji vyeo. Kama ilivyo kwa ajira, upandishwaji vyeo na uteuzi hutegemea sifa za muundo na utendaji mzuri, bajeti ya kugharamia mishahara na kulinda tange kwa kada husika ili kuwepo uwiano wa utendaji wa wasimamizi mahali pa kazi. Kutokana na misingi hii katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga nafasi 162,221 za kuwapandisha vyeo watumishi wenye sifa stahiki katika kada mbalimbali. Katika nafasi hizi, nafasi 2,044 zimetengwa kwa ajili ya kujaza mapengo mbalimbali ya vyeo vya uteuzi katika ngazi ya madaraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, uteuzi huu katika nafasi ya madaraka utapunguza kero ya kukaimu nafasi hizo kwa muda mrefu kama ilivyobainishwa na Waheshimiwa Wabunge katika kuchangia hoja yangu. Kutokana na kutolewa fursa hii, natoa rai kwa mamlaka za ajira na mamlaka nyingine zinazohusika, kuhakikisha kuwa zinaanzisha michakato hiyo mapema na kwa kuzingatia vigezo vilivyobainishwa katika miongozo mbalimbali iliyotolewa inayohusu uteuzi wa watumishi kushika madaraka. Pale ambapo hakuna watumishi wanaokidhi vigezo hivyo, waajiri wasisite kuomba kuhamishiwa watumishi wenye sifa stahiki kutoka maeneo mengine katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la nyongeza ya mishahara nalo limezungumzwa na wachangiaji wengi, suala hilo nalo ni la kibajeti na limeangaliwa kwa mapana yake.

Kutokana na umuhimu, Serikali inakusudia kutoa nyongeza ya mwaka kwa mujibu wa kanuni za utumishi wa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine lililozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge ni kuhusiana na mapambano dhidi ta rushwa. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa Serikali itaendelea kuimarisha vita dhidi ya rushwa. Hatua hizo ni pamoja na kuimarisha uadilifu, kuhakikisha viongozi na watumishi wa umma wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia viapo vya uadilifu na kuwajibika kwa matokeo ya kazi na maamuzi yao ili kuondokana na matumizi mabaya ya madaraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hatua hizi, Serikali itaendelea kuiwezesha TAKUKURU kutekeleza majukumu yake kwa kuwajengea uwezo watumishi wake, hasa katika maeneo ya uchunguzi, uendeshaji kesi za rushwa na ufisadi na kujenga ofisi hatua kwa hatua katika Wilaya mpya ambazo hazina ofisi za taasisi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maadili ya viongozi, Serikali itaendelea kujenga mifumo mbalimbali ya taratibu za kazi zinazoendana na mabadiliko ya teknolojia kwa kuwa ndio msingi mkuu wa uboreshaji wa utawala bora. Tutaendelea kuimarisha mfumo wa kufuatilia tabia na mienendo ya viongozi wa umma kwa njia ya kisasa zaidi ili waweze kujiepusha na vitendo vizivyo vya kimaadili.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa rai kwa viongozi wote kuwa mienendo bora ya uzalendo na hali ya juu kwa kuwa maendeleo yanatokana na mwelekeo bora wa viongozi. Viongozi wajenge tabia ya kujiuliza katika kila jambo kuwa wayafanyayo hayaleti mgongano wa maslahi?

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya Wabunge waliochangia walionesha wasiwasi kuhusu usalama wetu na shughuli za Idara ya Usalama wa Taifa. Idara hii hutekeleza majukumu kwa mujibu wa Sheria ya Usalama wa Taifa Namba 15 ya mwaka 1996. Kwa mujibu wa kifungu cha 4 cha sheria hii, majukumu ya msingi yaliyoainishwa ni kukusanya taarifa, kuchambua na kuishauri Serikali ipasavyo juu ya hatua za kuchukua ikiwemo usimamizi wa rasilimali za nchi. Aidha, kwa mujibu wa kifungu cha 5(a) Idara hii haihusiki na usimamizi wa sheria (law enforcement) kwa kuwa kwa mujibu wa mgawanyo wa majukumu, miongoni mwa vyombo vya ulinzi na usalama jukumu hili ni la mamlaka nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa naomba nichukue nafasi hii kufafanua Sheria ya Usalama wa Taifa inasema nini. Usipojua kazi za Idara ya Usalama wa Taifa utawapa lawama kwa shughuli ambazo si zao. Nataka kurejea sheria inasema nini, kifungu cha 5(1)(a), nataka kusoma kwa kiingereza halafu ntaeleza maana yake nini kwa kiswahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kubwa ya Usalama wa Taifa kwa mujibu wa sheria iliyopitishwa na Bunge hili inasema hivi; “To obtain, correlate, and evaluate intelligence relevant to security, and to communicate any such intelligence to the Minister and to persons whom, and in the manner which, the Director-General considers it to be in the interests of security.”

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ndiyo kazi kubwa ya chombo cha usalama nchi yoyote ile; kukusanya habari na kuishauri Serikali iliyopo madarakani. Sasa yale mnayosema wanatukamata ovyo, wanafanya hivi, nataka niseme mafungu mengine mawili sheria inasema nini. Namba mbili inasema; “It shall not be a function of the Service,” haitakuwa shughuli ya Idara kufanya mambo yafuatayo, moja; “To enforce measures for security,” (haitatumia mabavu kumkamata mtu ili ku-enforce security), sheria ndivyo inavyosema. Pili, nilikuwa nawasikiliza muda wenu basin a mimi mnisikilize. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili inasema haitakuwa kazi ya Idara ya Usalama, kwa kiingereza; “to institute surveillance of any person or category of persons by reason only of his or their involvement in lawful protest, or dissent in respect of any matter affecting the Constitution, the laws or
the Government of Tanzania” (haitakuwa kazi ya Idara ya Usalama kufuatilia mhalifu, haitakuwa kazi ya Idara ya Usalama).

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona niiseme hiyo kwa sababu mazungumzo mengi yaliyozungumzwa hapa yameelekezwa huko. Mtu ameuawa it is a police case, mtu amepotea it is a police case, hakuna nchi ambayo Idara ya Usalama inashughulika kukamata wahalifu. Inawezekana mnatumia hayo kujenga hoja zenu, lakini sheria ndivyo inavyosema. Kama mnataka wawe wanafanya hayo mnayoyataka leteni sheria hapa mbadilishe watafanya. Mimi mtumishi wa Bwana nitatenda kama Bwana anavyotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Idara hii hutekeleza majukumu kwa mujibu wa Sheria ya Usalama kama nilivyosema. Kwa mujibu wa kifungu cha 14 cha sheria hii majukumu ya msingi yaliyoainishwa ni kukusanya taarifa, kuchambua na kuishauri Serikali ipasavyo juu ya hatua za kuchukua ikiwemo usimamizi na rasilimali za nchi. Aidha, kwa mujibu wa kifungu cha 5(2)(a) Idara hii haihusiki na usimamizi wa sheria (law enforcement) kwa kuwa kwa mujibu wa mgawanyo wa majukumu miongoni mwa vyombo vya ulinzi na usalama jukumu hilo ni la mamlaka nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mgawanyo huu si sahihi kuihusisha Idara hii na matukio ya uhalifu yanayotokea kwa nyakati tofauti. Aidha, uhalifu kama huu hauikumbi Tanzania peke yake bali upo katika mataifa mengine na uchunguzi wake huchukua muda. Ipo mifano hai inayodhihirisha ugumu katika kubainisha wahalifu kwa kuwa wao hutumia mbinu mbalimbali. Waheshimiwa Wabunge watakumbuka jinsi Serikali ilivyokabiliana na uhalifu kama huo katika Wilaya ya Rufiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge kuiunga mkono Serikali katika mapambano dhidi ya uhalifu wa aina yoyote na wajiepushe kutoa matamko yanayoweza kuchochea uvunjifu wa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ofisi yetu inazo programu mahususi zinazochangia jitihada za Serikali katika kupambana na umaskini. Programu hizi hutekelezwa kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), Programu ya Kurasimisha Rasilimali za Wanyonge (MKURABITA) na Mfuko wa Rais wa Kujitegemea. Serikali itaendelea kutekeleza programu hizi ili kupunguza kiwango cha umaskini nchini. Aidha, Serikali itaendelea kuhakikisha wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya maskini ili kuhakikisha kuwa wanaonufaika ni wale tu wanaostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kueleza maelezo hayo kwa utangulizi, ninaomba sasa kupitia hoja sitozipitia zote ambazo zimejitokeza katika mjadala wa Wizara yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wajumbe wamesema kuna ukiukwaji wa misingi ya utawala bora kwa kutumia macho, vitendo vya mauaji, utekaji nyara, kupigwa watu na upendeleo mwingi. Hapa majibu tunasema Serikali haiungi mkono vitendo vyote vya ukiukwaji wa misingi ya utawala bora na ndiyo maana kila vitendo hivi vinapojitokeza Serikali huchukua hatua mara moja kwa mujibu wa sheria za nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika hivyo, Serikali inaomba wanasiasa na wananchi kwa ujumla kuunga mkono hatua za Serikali zinazochukuliwa katika Jeshi la Polisi lenye dhamana ya usalama wa raia. Jeshi lenye dhamana ya usalama wa raia ni Jeshi la Polisi, si Idara ya Usalama. Hata hivyo, ni jukumu la kila raia kutoa taarifa sahihi kwa Jeshi la Polisi ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kumekuwepo na ukiukwaji mkubwa wa sheria za nchi na Katiba ya nchi, mfano kuzuia mikutano ya hadhara, kukosekana kwa uhuru wa mawazo, wanaokosoa Serikali au kuishauri wanapata misukosuko na wengine wanapoteza, watumishi wa kiroho kupata misukosuko baada ya kudai kuwepo kwa Katiba Mpya au Serikali kukosolewa kwa maslahi, magazeti kufungiwa na waandishi kutozwa faini kwa sababu ya kutoa taarifa zisizopendeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hapa napenda kujibu hoja hii kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, si kweli kuwa Serikali inakiuka sheria ya nchi na Katiba katika kutekeleza majukumu yake. Mtu yeyote au taasisi inayoona inanyimwa haki ya kisheria na Kikatiba ina nafasi ya kupeleka malalamiko yake kwenye vyombo vinavyotoa haki ambayo ni mahakama. Aidha, pamoja na uhuru huo kuwepo, ufanyike kwa mujibu wa sheria za nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu magazeti kufungiwa, hufanyika kwa mujibu wa sheria zilizopitishwa na Bunge. Tena Sheria ya Magazeti ilikuwepo ya mwaka 1976 tukailalamikia, Bunge hili limepitisha Sheria ya Magazeti, ndani ya Sheria ile ya Magazeti kuna chombo kinaitwa Content Committee ya senior citizens, kazi yao wao ni kufuatilia vyombo vya habari, yule ambaye amekwenda kinyume na maadili anaadhibiwa. Wale watu wameadhibiwa na Content Committee, Waziri anashauriwa na Content Committee, anapofunga Waziri anafungia kwa mujibu wa sheria na waliomshauri wamo ndani ya Sheria ya Vyombo vya Habari iliyopitishwa na Bunge hili linaloendelea leo hapa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la watumishi wa kiroho kupata misukosuko, Serikali haina ushahidi wa jambo hilo; na mimi nasema suala la watumishi wa kiroho ningependa sana nilichangie lakini sitaki kuchangia, ila niseme tu kifupi; ukitaka kumshauri mzee wako huitishi mkutano wa hadhara ukasema ninamshauri baba, hakuna njia ya kumfikia huyo baba yako kimya kimya? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la watumishi wa kiroho kupata misukosuko, Jeshi la Polisi linafanya uchunguzi wa uhalifu wowote bila kujali umefanywa na nani.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine lililozungumzwa sana, ni sheria ipi inayowapa mamlaka Wakuu wa Mikoa na Wilaya kuwaweka watu ndani saa 24 na ni hatua zipi zimechukuliwa na Wakuu wa Mikoa na Wilaya inapobainika kwamba wananchi wamewekwa ndani kimakosa na hili nataka nilieleze.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wamepewa mamlaka ya kisheria, Regional Administration Act ya mwaka 1997 (Sheria ya Tawala za Mikoa mwaka 1997) imewapa madaraka kumuweka mtu yeyote ndani anayebainika kutenda kosa lolote lenye kuhatarisha amani na utulivu wa jamii husika. Anayeona hakutendewa haki, kwamba hakuwekwa kwa misingi hiyo ana ruhusa ya kulalamika kwa wakubwa wake wa kazi, hakuridhika, ruhusa kwenda mahakamani.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kwa kuwa Mkoa wa Kigoma umekuwa ukitoa malalamiko yake kwa Serikali na yamekuwa yanapuuzwa, hususani kupotea kwa Diwani na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kibondo bila maelezo yoyote, wananchi watajichukulia hatua na kufanya wanavyoona inafaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nadhani ndugu yangu Mheshimiwa Zitto pale ulikuwa unatuhimiza tu kwamba jambo hili tulifanyie kazi, lakini ninavyomuelewa Mheshimiwa Zitto alivyo msomi, kijana, anaipenda nchi, ana akili, simuoni Mheshimiwa Zitto anahamasisha watu kuchukua sheria mkononi, yale maeneo aliyaweka tu kutuhimiza watu wa Serikali kwamba please take action. Point noted, tumeipokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo yake, majibu yake; Serikali haipuuzi malalamiko ya upotevu wa watu nchini ikiwemo Diwani na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kibondo kama anavyodai Mheshimiwa Mbunge. Suala la kupotea kwa Diwani huyo lilisharipotiwa katika Jeshi la Polisi na uchunguzi unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, na tena hapa mimi nataka nimpongeze ndugu yangu Mheshimiwa Zitto, huyu Diwani anayemtetea tumtafute mpaka tumpate, wala sio wa chama chake ACT, ni Diwani wa CCM, inaonesha jinsi alivyo mzalendo anavyopenda haki itendeke kwa kila mtu, sasa uendelee hivyo hivyo mdogo wangu Mheshimiwa Zitto, usiyumbe katika mengine, endelea hivyo hivyo. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inasisitiza mwananchi mwenye taarifa kuhusu jambo hili ajitokeze kusaidia polisi ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa. Kama nilivyosema mwanzo, this is another police case, kesi nyingine ya polisi, si ya vyombo, kesi nyingine ya polisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Selasini; kuna mwandishi wa habari aitwaye Cyprian Musiba amekuwa akitoa matamko hatarishi katika vyombo vya habari yakiwemo na magazeti anayoyafanyia kazi lakini Serikali ikiwemo na Idara ya Usalama wa Taifa imekaa kimya na haijatoa tamko lolote la kubeza, hivyo wananchi waelewe vipi kama matishio hayo yana kibali cha Serikali?

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Selani, nataka nikueleze kuwa sheria iliyotungwa na Bunge hili inataka Idara ya Usalama wa Taifa ifanye kazi zake kwa faragha. Kwa hiyo, hii hoja uliyoitoa kwamba hata Idara ya Usalama wa Taifa imekaa kimya, nilishawahi kueleza humu ndani siku moja, hautawahi kusikia hata siku moja taarifa imetolewa na Msemaji wa Idara ya Usalama wa Taifa. Kwa hiyo, suala la wao kuwaita watu na kusema jamani sisi tumeishauri Serikali hivi, huyu bwana tumemchukulia hatua hii, si kazi yao, kazi yao ni kukusanya habari, kuishauri Serikali, wamemaliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa mujibu wa sheria ya nchi Jeshi la Polisi ndilo linalopewa dhamana ya kufanyia uchunguzi matamko yote yenye kuhatarisha usalama wa raia na ambayo ni makosa ya jinai na pale inapojiridhisha huwapeleka wahusika mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Idara ya Usalama wa Taifa kukaa kimya ni utekelezaji wa sheria, kama nilivyosema, wanafanya kazi yao kwa faragha. Hujawahi kuwasikia na hutawasikia wanaita press conference. Hata hivyo, mtu yeyote ambaye ataona ameathiriwa na matamko hayo ana haki ya kuyapeleka malalamiko yake kwa Jeshi la Polisi ili hatua zaidi ya uchunguzi wa kisheria iweze kuchukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Almas Athuman Maige; Idara ya Usalama wa Taifa itoe semina kwa Waheshimiwa Wabunge ili waweze kupata uelewa juu ya kazi na shughuli za Usalama wa Taifa. Mimi nakushukuru sana ndugu yangu Mheshimiwa Maige, kama nilivyoeleza tangu mwanzo, ukifuatilia maelezo yangu juu ya Idara hii utaona kwamba tunawauliza maswali inawezekana wakati mwingine kwa kutokufahamu na mimi tangu nimeingia katika Wizara nilipoliona hivyo, ombi limepokelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali ilishapeleka maombi Ofisi ya Spika kuhusu kufanyika kwa semina hiyo katika kipindi hiki cha Bunge linaloendelea ili tuelewane wao wanafanya nini. Mpate muda wa kuuliza maswali, mjiridhishe ili tuendelee kuwahoji yale yanayowahusu, yale yasiyowahusu tushughulike na wanaohusika.

Mheshimiwa Naibu Spika, utawala bora safari hii ilikuwa ni Idara ya Usalama tu; utendaji kazi wa Idara ya Usalama wa Taifa hauridhishi, je, inacho Kitengo cha Economic Intelligence ambacho kingeweza kutoa ushauri kwa Serikali juu ya masuala mbalimbali ya kiuchumi yakiwemo ya usimamiaji wa miradi na mikataba ya uwekezaji? Ameuliza ndugu yangu Mheshimiwa Ngwali hapa, ametoka, basi lakini atasikia. Mheshimiwa Ngwali alikuwa Mjumbe machachari kwenye Kamati yangu, safari hii sijui amehama, sijamuona, na anatuhamasisha watu wa Serikali kufanya mambo mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, muundo wa Idara ya Usalama unatokana na majukumu yaliyobainishwa katika Sheria Namba 15 ya mwaka 1996 inayounda taasisi hiyo. Moja, anasema Usalama wa Taifa


hauridhishi; nataka nimhakikishie ndugu yangu Mheshimiwa Ngwali, nchi hii iko salama, jahazi linakwenda, limeshikwa na nahodha madhubuti, kazi yake yeye ajishikilie tu mawimbi yakija asije akaanguka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kama nilivyosema, shughuli zao hufanyika kwa faragha. Sasa muasisi wa Jamhuri ya Watu wa China, Mheshimiwa Mao Tse-Tung alisema hivi; “no research, no right to speak”. Jambo ambalo hujalifanyia utafiti, huna uhakika nalo usiliseme. Ndugu yangu Mheshimiwa Ngwali una uhakika gani kwamba hayo unayoyasema kwenye idara hayapo? Umeshawahi kuingia kule? Lakini kwa sababu shughuli zao wanafanya kwa faragha siwezi nikakujibu kwamba kitengo wanacho au hawana kwa sababu mila na desturi ya chombo cha usalama ni kufanya kazi kwa faragha. Lakini jibu la uhakika tu nililokupa ni hilo moja kwamba nchi iko salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi kwa TAKUKURU na Usalama wa Taifa, ndugu yangu Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, nakushukuru. TAKUKURU na Usalama wa Taifa waendelee kutumia utaalam na weledi kuishauri Serikali katika kukusanya mapato na matumizi ya fedha za umma; ushauri umepokelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri mwingine miradi ya maji Handeni Vijijini ina ubadhirifu wa rushwa. Tumeeleza hivi; Serikali imedhamiria kutokomeza rushwa nchi hii, kuondoa umaskini na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, TAKUKURU imekuwa ikifuatilia miradi ya maendeleo na nataka nikuhakikishe mpwa wangu, Mheshimiwa Mboni Mohamed Mhita, kwamba jambo ulilolitaja TAKUKURU ina taarifa nalo, inalifanyia kazi muda mwafaka ukifika tutachukua hatua. Tukiwaona kwamba baada ya utafiti hawana hatia tutawaacha, tukiona wana hatia hatua zitachukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, TAKUKURU wawezeshwe kuwa na ofisi nzuri na vitendea kazi ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi. Ndugu yangu Mheshimiwa Juma Selemani Nkamia, nakushukuru kwa kututetea.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ofisi za Serikali ziwe na ushirikiano na TAKUKURU ili kuepuka matumizi mabaya ya fedha za umma. Maelezo yake ni kuwa Serikali itaendelea kuiwezesha TAKUKURU kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa kuwapatia vitendea kazi na kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa kadri bajeti ya Serikali itakavyoruhusu. Hata hivyo, kwa mwaka huu wa fedha Serikali imepanga kujenga ofisi saba za Wilaya na mwaka 2018/2019 zitajengwa ofisi kumi. Kwa hiyo, ninaomba tu Waheshimiwa Wabunge na ndugu yangu Mheshimiwa Juma Selemani Nkamia na Mheshimiwa Emmanuel Papian basi mtuunge mkono, mpitishe bajeti hii ili ofisi zijengwe kama mnavyokusudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine inasema Serikali iandae utaratibu wa kuingiza somo la maadili katika mitaala ya elimu ya msingi na sekondari ili kujenga kizazi chenye maadili na uzalendo ambacho kitaelewa, kitachukia na kupinga vitendo vya rushwa. Nataka nishukuru kwa ushauri huo. Somo la maadili limeingizwa katika mitaala ya elimu ya msingi na masomo yanayofundishwa ni uraia na maadili. Kwa upande wa shule za sekondari somo la maadili linajitokeza katika masomo ya general studies na civics (uraia).

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mchakato wa kuanzisha mitaala ya somo la rushwa kwenye shule za sekondari unaendelea. Vilevile katika kuimarisha elimu ya maadili shuleni na vyuoni kumefunguliwa na vilabu vya maadili katika shule na vyuo mbalimbali. Ushauri tumeupokea, tunaufanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine, Sekretarieti ya Maadili inapowataka viongozi kuwasilisha fomu waeleze pia nyaraka nyingine zote zinazotakiwa kuwasilishwa ili ziwasilishwe kwa pamoja. Hoja tumeipokea hitaji la nyaraka na mali za madeni ya viongozi wa umma hujitokeza pale sekretarieti inapotaka kufanya uhakiki wa matamshi ya rasilimali na madeni ya viongozi wa umma baada ya kupokea fomu hizo ili kuthibitisha ukweli wa tamko lililotolewa na kiongozi husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF). Zoezi la kutambua na kuandikisha kaya maskini katika maeneo ambayo hayakufikiwa katika awamu ya kwanza na mradi wa ruzuku kwa kaya maskini ifanyike mapema ili kaya maskini katika maeneno hayo yanufaike na mpango wa ruzuku. Takwimu zinaonesha yapo maeneno ya vijiji 4,408; mitaa 1,189; shehia 96 ambayo haijafikiawa katika awamu ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo ni kuwa utaratibu wa kufikia vijiji vyote ambavyo havijafikia umeandaliwa katika sehemu ya pili ya mpango wa kunusuru kaya maskini tunaotarajia kuanza mwaka 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kwamba Serikali ianze maandalizi ya kuwezeza mpango wa ruzuku kwa kaya masikini kuwa endelevu; ushauri umetoka kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala ushauri umepokelewa. Hata hivyo TASAF inakitengo maalumu cha kukuza uchumi wa kaya ambacho kinaandaa kaya na walengwa kutoka kwenye mpango wakiwa tayari na stadi na kuendelea na maisha yao pale mpango ukapokwisha au watakapohitimu kwenye mpango ili kuwapisha wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ni kwamba Halmashauri zitumie maofisa maendeleo ya mamii ili kuelimisha wanufaika wa mpango wa ruzuku wa kaya maskini namna wanavyoweza kutumia sehemu ya ruzuku hiyo kujikwamua.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika baadhi ya maeneo walengwa wamenufaika kwa kuanzisha kilimo na ufugaji wa kutumia sehemu ya ruzuku. Maelezo ya Serikali ushauri tumeupokea, kwa kiasi kikubwa mpango wa kunusuru kaya maskini unafanya kazi na Maafisa Maendeleo ya Jamii ambao wengi wao ni waratibu wa mpango katika ngazi za Halmashauri. Serikali itahakikisha kuwa katika maeneo ambayo bado hayaajanza kuwatumia watumishi hao wawashirikishe katika shughuli za mpango.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ni kwamba Serikali iwafuatatilie kwa karibu viongozi wanasiasa katika vitongoji, vijiji na kata kwani yako malamiko ya baadhi ya wananchi kuwa baadhi ya viongozi wanasiasa wanatambua na wahitaji kwa upendeleo bila kuzingatia vigezo. Maelezo ya Serikali, utambuzi wa kaya maskini katika maeneo yaliyoko kwenye mpango hufanywa na wananchi katika mikutano ya hadhara ambayo inasimamiwa na viongozi wa vijiji, miji na Halmashauri. Hata hivyo yanapotokea malalamiko uhakiki hufanyika na kuwaondoa wasiokuwa na vigezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hao wanaonufaika sasa na mpango wa TASAF, tulipoanza utekelezaji baadhi ya maeneo wananchi walilalamika, tukatumia vyombo vya Serikali katika ngazi zinazohusika na walipothitisha kwamba ni kweli wameongopa wametolewa katika mpango wa TASAF. Vilevile watumishi wa Serikali waliokuwa wamewasajili watu ambao wanajua hawakuwa na sifa ya kusajiliwa na wao wamechukuliwa hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba Serikali iongoze bajeti ya MKURABITA na kutoa kikamilifu na kwa wakati ili kuongeza kasi ya upimaji na urasimishaji wa ardhi na biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ya Serikali ni kuwa Serikali imeendelea kuona umuhimu wa shughuli za MKURABITA na kuendela kutenga fedha katika bajeti kulingana na upatikanaji wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imetenga bilioni 4.3 ambapo hadi kufikia jumla ya shilingi bilioni 2.4 sawa na asilimia 57 zimepokelewa na kutumika. Aidha, mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga shilingi bilioni 4.4 kwa ajili ya shughuli za MKURABITA.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutoa fedha kama zinavyotengwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine; katika utekelezaji wa shughuli za MKURABITA ambao umewanufaisha wengi wakiwemo wananwake bado vijana hawajanufaika kwa kiwango cha kuridhisha na mpango huu. Serikali ifanye utaraibu utakaowezesha vijana wengi kunufaika. Maelezo ya Serikali katika mwaka wa fedha 2018/2019 MKURABITA imejipanga kutumia fedha ya kituo kimoja cha urasimishaji kuwawezesha vijana kuwa wabunifu kuchangia katika upatikanaji wa ajira na hivyo kuwa wameshiriki katika kujenga uchumi wa Taifa. Aidha, jumla ya vituo vitano vya usafirisahji biashara vitaanzishwa Tanzania Bara na viwili Tanzania Zanzibar, vituo hivyo tumevitaja.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine, benki na taasisi za fedha zikielimishwa kuhusu ardhi na hati ya haki miliki za kimila kutumika kama dhamana ya mkopo zitatoa mikopo kwa wananchi wanaomiliki ardhi kwa hati hizo. Maelezo ni kuwa kwa sasa benki na taasisi nyingine za fedha zinakubali hati miliki za kimila tutumika kama dhamana ya mkopo na pale itakapotokezea kwamba kuna benki inakataa Waziri wa Nchi anayeshughulika na masuala ya Utumishi na Utawala Bora nikiletewa habari nitafanyia kazi.

Mhehsimiwa Naibu Spika, Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa inasema Mfuko wa Rais wa Kujitegemea (PTF) uwezeshwe kifedha kutanua wigo wa shughuli zake nchini na hivyo kuwafikia wanawake na vijana. Majibu ya Serikali ni kuwa katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imeongeza bajeti ya maendeleo ya Mfuko wa Rais wa Kujitegemea kutoka shilingi milioni 500 mwaka 2017/2018 hadi shilingi bilioni 1.7 mwaka wa fedha 2018/2019 ili kutatua wigo wa kuwafikia wanawake na vijana wengi zaidi. Aidha, Serikali itaendelea kuuwezesha mfuko huu kulingana na uwezo na itaendelea kushirikiana na mamlaka ya Seriakli za Mitaa na wao waendelee kutoa mikopo kwa walengwa waliopo katika eneo lao.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine inasema Serikali kupitia Taasisi ya Uongozi (Uongozi Institute) itoe mafunzo ya uongozi na utawala kwa viongozi walioteuliwa ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria kanuni na miongozo ya kiutendaji, na hivyo kuepusha migogoro isiyo na lazima ambayo inaweza kuibuka. Hii imetoka kwenye Kamati ya Kudumu ya Utawala na Serikali za Mitaa. Majibu ya Serikali ni kuwa Serikali kupitia taasisi mbalimali ikiwemo Uongozi Institute ina jukumu la kutoa mafunzo ya uongozi na utawala bora kwa viongozi wanaoteuliwa ikiwa ni pamoja na viongozi wa Mikoa, Wilaya, Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria kanuni na miongozo ya kiutendaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miezi nane iliyopita mafunzo yaliyohusisha mahusiano ya kiutendaji kati ya viongozi wa siasa na watendaji, utawala bora na uwajibikaji maadili na kujenga sifa binafsi za kiuongozi yalitolewa kwa Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa kupitia Taasisi ya Uongozi. Aidha, taasisi imeandaa mafunzo ya aina hiyo kwa ajili ya wakuu wa mikoa na makatibu tawala wa mikoa. Serikali itaendelea kutoa mafunzo kwa viongozi wanaoteuliwa pale inapohitajika kwa lengo la kuimarisha uhusiaono wa kiutendaji wa kuboresha huduma za jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ni ile inayohusu kwamba Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kiwezeshwe kukamilisha awamu ya mwisho ujenzi wa jengo ambalo linaendelea katika campus ya Tabora. Maelezo ya Serikali ni kuwa Kamati inatambua umuhimu wa kukamilisha ujenzi wa jengo lililopo katika campus ya Tabora, ujenzi huu unatekelezwa kwa kutumia mapato ya ndani ya chuo. Aidha, katika mwaka wa fedha kiasi cha shilingi milioni 500 kimetengwa, shilingi milioni 800 kwa mwaka wa fedha zimetengwa kwa ajili ya mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niihakikishie Kamati inayonilea hapa Bungeni ya Katiba na Utawala kwamba mimi Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii nitasimamia na kuhakikisha kuwa jengo lile linakamilika ili Tabora Secretarial College ambayo ndiyo Secretarial College ya kwanza ya Serikali katika nchi hii kuirudishia hadhi yake. Ndiyo maana hata katika mafunzo ya degree ya ma-secretary tumeanza Dar es Salaam, lakini tunafanya maandalizi Tabora ili Tabora Secretarial College itoe degree ya u-secretary kwa sababu ndicho chuo cha mwanzo cha ma-secretary cha Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine Serikali iangalie uwezekano wa kuridhia Mamlaka za Serikali za Mitaa kuajiri bila kibali na kuziachia kuendesha mchakato wa ajira kwa watumishi wa kada za afya. Maelezo ya Serikali ni kuwa kuajiri watumishi baada ya kupata kibali na matakwa ya Sheria ya Utumisha wa Umma Namba Nane ya mwaka 2002 pamoja na kanuni zake. Aidha, Bunge katika Sheria ya Mabadiliko Sheria Mbalimbali (Written Laws Miscellaneous Amendment Namba Mbili ya mwaka 2013 iliifanyia marekebisho Sheria ya Utumishi wa Umma Namba Nane ya mwaka 2002. Katika mabadiliko hayo Katibu Sekretarieti ya Ajira amepewa mamlaka ya kukasimu uendeshaji wa mchakato wa ajira kwa waajiri katika tangazo la Serikali la mwaka 2014 ambapo Mamlaka za Serikali za Mitaa zimekasimiwa kuendesha mchakato wa ajira wa kada za chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachosema kwamba ombi hili limepokelewa na Serikali, Halmashauri zimekasimiwa kufanya huo mchakato wa mahojiano mpaka ajira, lakini kila inavyotokea hivyo, kwa sababu kule Wilayani tunafahamiana huyo mtoto wa mjomba, huyu mtoto wa fulani, Sekretarieti ya Ajira inatuma wawakilishi katika mchakato huo ili kuhakikisha kwamba haki inatendeka. Kwa sababu haki isipotendeka lawama si Halmashauri lawama ni ya Waziri mwenye dhamana ya Utumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine imelezwa kwamba kuna upungufu mkubwa wa watumshi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa hususani kada ya walimu wa shule za msingi, walimu wa masomo ya sayansi, hisabati, watumishi wa kada ya afya, watendaji wa vijiji, watendaji wa mitaa watendaji wa kata, maafisa ugani wa kilimo na mifugo na watumishi wa kada nyinginezo. Majibu ya Serikali ni kuwa katika kila mwaka wa fedha Serikali imekuwa ikitenga nafasi za ajira mpya kulingana na mahitaji yake pamoja na vipaumbele vyake hususani katuka maeno ya elimu kilimo, afya, mifugo na uvuvi kutokana uwezo wa kibajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia Machi, 2018 Serikali imeajiri watumishi zaidi ya 18,000 ili kukabiliana na upungufu wa watumishi katika sekta za kipaumbele na zenye upungufu mkubwa kwa watumishi. Aidha, Serikali imepanga kuajiri watumishi 52,436 katika mwaka wa fedha 2017/2018 wengi wao wakiwa wa idara ya elimu afya na serikali za mitaa. Hawa tunaowaajiri mlishapitisha katika bajeti iliyopita, ni tofauti na wale 49,000 tunaotaka kuwaajiri katika bajeti inayokuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo katika mwaka wa fedha 2018 Serikali imetenga nafasi ya ajira jumla 49,536 na hapa Waheshimiwa Wabunge kwa faida ya Bunge letu na faida ya wananchi wapate kufahamu; ni kwamba zoezi la ajira lilisimama wakati umeanza mchako wa kuhakiki vyeti. Ilionekana si busara unampandisha mtu leo halafu kesho unaambiwa cheti fake unaondoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi lile la kutambua vyeti fake limekamilika ndiyo maana Serikali ikaanza kuwaajiri watu mbadala wale waliondolea zoezi hilo nalo sasa karibu limekamilika tutaendelea na ajira mpya kama nilivyosema, 52,000 wa mwaka jana 2017 na mwaka ujao Serikali imejipanga kuwaajiri 49,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ya msingi sana, kwamba Serikali ifungue milango ya uhamisho kwa watuishi ambao wanahitaji kuungana na familia pale mwenza mmoja anahamishwa ili kuondoa usumbufu wa familia. Aidha, kumekuwa na usumbufu mkubwa wa mtumishi anapotaka kuhama na kuambiwa atafute mtu wa kubadilishana naye, na kwamba asipopatikana huyo mtumishi anakosa haki ya kuhama. Je, huo ni wajibu wa mtumishi au Serikali kutafuta jinsi ya kujua ni wapi mtumishi huyo atapangwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo ya Serikali ni kama ifuatavyo; Serikali haijafunga milango ya watumishi wale wanaotaka kuhama ili kuungana na familia zao au kwa sababu nyingine zozote zile za msingi. Aidha, maelekezo yametolewa kwa waajiri kupitisha maombi ya watumishi yaliyowasilishwa kwao ili mradi yamezingatia taratibu zilizopo kwa kuwa si sera ya Serikali kuzuia uhamisho wa watumishi katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako Tukufu naomba nitoa maagizo haya kwa mamlaka zote za Serikali za ajira katika nchi hii. Malalamiko makubwa waliyonayo watumishi wa umma ni kwamba wakiomba kuhama anapotakiwa kupitisha barua kwa mkubwa wake wa kazi wanawakatalia! Wanawakatalia! Sasa naomba kulieleza Bunge hili tukufu, mwenye mamlaka ya kumkatalia uhamisho ni yule anayeandikiwa barua, wewe uliyeandikiwa pale kupitia kwa, kiswahili sanifu kabisa kupitia kwa, wakishasema kupitia kwa wewe si mwamuzi wa mwisho, ndiyo maana inaandikwa kupitia kwa, peleka barua kwa mwajiri ili mwajiri apate kuamua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natembelea mikoani nimekwenda mkoa mmoja naambiwa hii ofisi yetu haijapitisha barua ya mtu kuhama hata siku moja.

Mimi ninasema, mimi ndiye Waziri wa Utumishi wa Umma, nikibaini kuna kiongozi wa utumishi anakataa kupitisha barua isinifikie mimi isimfikie Katibu Mkuu Kilimo, isimfikie Waziri Mkuu nitamshughulikia kwa mujibu wa sheria na taratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitafanya hivyo kwa sababu mtu huyo amejichukulia madaraka yasiyo yake, hukuandikiwa wewe barua umeandikwa kupitia kwa, sasa kupitia kwa wewe ndiyo unaamua? Sasa mimi niliye juu hapa nitafanya kazi gani kama wewe unaniamulia?

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja imetolewa hapa na Mheshimiwa Ahmed Juma Ngwali, sasa rafiki yangu mwenyewe yuko wapi, amenikimbia? Anasema Serikali ilete muswada wa sheria wa kuibadili eGA kuwa mamlaka ili kuwa na nguvu za kisheria kusimamia na kudhibiti utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, majibu kuhusu Serikali Mtandao na je, Wakala wa eGA umetengewa kiasi gani kukabiliana na teknolojia inavyobadilika? Swali zuri na ushauri umepokewa ndugu yangu Mheshimiwa Ngwali, mchakato wa kutunga sheria ya kuibadili Wakala wa Serikali Mtandao kuwa mamlaka tayari umeanza Serikalini, na hapa mimi nataka niishukuru Kamati yangu ya Utawala na Serikali za Mitaa, wao wamejenga hii hoja ndani ya Kamati wamenishauri mimi Waziri ninayehusika tuanze mchakato wa kuibadili kuwa mamlaka ya Serikali mtandao.

Mheshimiaw Naibu Spika, kazi hiyo imeshaanza mimi natekeleza kama nilivyoagizwa na Kamati yangu; mimi mtumishi wa Bwana, nitatenda kama Bwana anavyotaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha katika bajeti ya mwaka wa fedha 2018/2019 Fungu 22 Wakala wa Serikali Mtandao imetengewa kiasi cha fedha shilingi bilioni nne kwa ajili ya miradi ya maendeleo na shilingi bilioni 3.6 kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Fedha hizi pamoja na mambo mengine zitaanzishwa kituo cha utafiti, ubunifu wa maendeleo ya Serikali Mtandao Makao Makuu Dodoma ili kukabiliana mabadiliko ya kiteknolojia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho katika hoja ambazo naomba kuzisemea leo, kwamba Serikali iwezeshe kikamilifu Idara Kumbukumbu ya Nyaraka za Taifa kwa ajili ya kufanya tafiti, kukusanya na kuhifadhi taarifa na kumbukumbu muhimu katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Miongoni mwa njia ya kukusanya taarifa hizo ni kutembelea na kuhoji watu wenye umri mkubwa ambao wameshuhudia mambo mengi ambayo ni muhimu kwa taifa na vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo ya Serikali ni kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kukusanya na kuhifadhi kumbukumbu na nyaraka ili kuhifadhi urithi andishi kwa ajili vizazi vya sasa na vizazi vya maendeleo ya Taifa letu. Katika kutekeleza jukumu hili Serikali imekuwa ikitenga fedha kupitia bajeti ya kila mwaka kulingana na uwezo wa kifedha kwa lengo la kuiwezesha idara kutekeleza majukumu yake. Kutokana na fedha hizo idara imekuwa ikitekeleza kazi mbalimbali ikiwemo kufanya tafiti kutambua, kukusanya na kuhifadhi kumbukumbu na nyaraka zenye umuhimu kutoka taasis za umma katika sekta mbalimbali na za watu binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya ni katika maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyasemea. Taratibu na mila za Bunge zinataka niyasome majina ya watoa hoja nilikuwa na mashaka ya muda, ukiruhusu nitawasoma waliotoa hoja, usiporuhusu nitawaweka wataingia katika kitabu chetu cha kumbukumbu ya Hansard…

NAIBU SPIKA: Waweke waingie kwenye kumbukumbu kwa sababu kanuni zetu haziruhusu kutaja majina, usiwaite kwa sababu kanuni zetu haziruhusu waingine kwenye Hansard.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maelekezo, wote mliotoa hoja hizi majina yenu tutayaingiza kwenye Hansard.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge kama mtakavyoona tumejitahidi kuangalia maeneo yapi Wabunge walitaka maelezo, maeneo yapi lazima yafanyiwe kazi. Mimi nataka niseme kwa naiba ya Serikali nataka niwashukuru Wabuge wote kwa michango yenu.

Mimi Waziri hii ndiyo bajeti yangu ya kwanza, lazima niseme nimenufaika sana na michango mliyotoa Wabunge imetuwezesha, mmetuboresha, mmetuweka kuwa imara ili utendaji wa kazi ndani ya Serikali ya Tano uweze kuwa na ufanisi zaidi.

Sasa naomba kuhitimisha maelezo yangu kwa kuomba Waheshimiwa Wabunge kuunga mkono hoja hii ili kuiwezesha ofisi yangu kutekeleza majukumu ya Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na taasisi zake kwa ufanisi katika mwaka ujao wa 2018/2019. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika,
nakushukuru kunipatia nafasi kufafanua baadhi ya mambo ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa Wabunge katika masuala yanayohusiana na Wizara yangu.

Mheshimiwa Spika, pili, nichukue nafasi hii kushukuru sana kwa uongozi madhubuti ambao Wizara yangu inapata kutoka katika Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa ambayo ndiyo Kamati inayohusika na Wizara yangu. Wanafanya kazi nzuri, Mheshimiwa Rweikiza, Makamu wake Mheshimiwa Mwanne Mchemba, pamoja na Wajumbe wote wa Kamati ile tunakwenda vizuri sana na mafanikio tunayoyapata katika Wizara yetu ni mafanikio pia yaliyochangiwa na Kamati hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikianza na suala la uhaba wa watumishi, nadhani juzi nililifafanua na leo nitalisema kwa kifupi sana. Tunakubadili kwamba mwaka jana walimu wengi wamestaafu na wengine wameaga dunia, nikasema tayari tuliomba tupate takwimu hizo kutoka Wizara ya Elimu wamekwishatuletea tunangoja za TAMISEMI nao watuletee. Tunataka kwanza kujaza mapengo hayo, tukijaza mapengo hayo maana yake ni kwamba hakuna gharama ya mishahara mipya, tena kwa uhakika ni kwamba hata mishahara tutakayolipa ni pungufu kwa sababu hawa watakaowaajiri ni wapya, wale waliostaafu walikuwa na mishahara mikubwa kuliko tunaotaka kuwaajiri. Kwa hiyo, haitupi mashaka na hatupati shida kutamka kwamba tutajaza mapengo kwanza baada ya hapo tutaangalia hali ya uchumi wetu tutakuwa na ajira mpya. Kwa hiyo, nilitaka niseme hivyo kwa upande wa watumishi hasa upande wa elimu na afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini juzi pia nilipochangia nilisema kwa wimbi hili la kwamba tunajenga zahanati, vituo vya afya na hospitali kila mahali, msingoje mmalize kabisa, wale ambao wanajua kwamba zahanati au kituo chetu cha afya tutafungua tarehe fulani, tuleteeni maombi hayo ili jengo likikamilika, vifaatiba vikipatikana kazi ya tiba ianze mara moja. Naomba wote mfanye hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine amezungumza ndugu yangu, Mheshimiwa Selasini kuhusu masuala ya utawala bora. Kauliza swali, je, hao tunaowateua tunawapekua? Kwa uhakika nataka nithibitishe tunaowateua kabla hatujakuteua tunajiridhisha, je, wewe raia, mwenendo wako, akili yako iko timamu, unaishi vizuri na watu, upekuzi tunafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili ambalo amelizungumza ambalo namuunga mkono na nataka niseme hii ni practice ya dunia nzima, utawala wa Rais mpya akiingia anafanya mabadiliko kwa jinsi anavyoona yeye inafaa. Nilitoa mfano siku moja mule ndani, ukienda Marekani kule mpaka wapika chai wale wote State House mfagizi, dereva, wote wanaondoka kupisha timu mpya. Sasa hili lililofanyika ni kwamba uteuzi umefanyika lakini namuunga mkono mdogo wangu Mheshimiwa Selasini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la mafunzo kwa wale wanaoteuliwa, jambo hili nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba tumelifanya. Tumefanya mafunzo kwa Wakurugenzi wa Halmashauri, Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala na sasa tumeshaandaa tayari mafunzo kwa Makatibu Tawala wa Wilaya, yatafanyika muda wowote kuanzia leo. Kila kitu wameshapelekewa, nauli na jinsi watakavyofika, wanangoja tu tuwaambie lini na wapi, watapata mafunzo kwa sababu ni muhimu sana hawa Maafisa Tawala wa Wilaya wakapata mafunzo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo amelizungumzia ni Regional Administration Act ya mwaka 1997, nataka nirudie tena kufafanua, ambayo inampa Mkuu wa Wilaya madaraka ya kumweka mtu ndani muda wa saa 24. Nataka nirudie, muda wa saa 24, lugha iliyozungumzwa pale ni kwa usalama wake. Kwa usalama wake maana yake, ameua mtu, jamaa zake wamekasirika wanataka kumpiga yule aliyeua, unamweka ndani kwa usalama wake. Sheria inasema akishamaliza saa zile 24 asubuhi lazima umpeleke Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mahali popote, nilisikia siku moja, Mkuu wa Wilaya kumweka mtu ndani muda wa saa 48 ni makosa kwa sababu sheria inampa yeye saa 24, Mkuu wa Mkoa amepewa saa 48. Nataka niwahakikishie Watanzania kupitia Bunge hili, mimi ni Waziri wa Utawala Bora, kazi zangu sifanyi kwenye mkutano wa hadhara na kusema leo tumefanya haya na haya, watumishi wote wa umma wanahusika na utawala bora. Kwa hiyo, inapokuja kwenye suala la utawala bora mimi ni Waziri wa Wizara zote, tunafuatilia tunachukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkuu wa Mkoa saa zake ni 48, anaweza akamweka saa 24 akipenda. Nachotaka kusema siyo lazima wewe umuweke mtu ndani kama ni criminal offence OCD yupo, kama ni suala la Uhamiaji, Afisa Uhamiaji yupo, kama amekwepwa kodi mtu wa TRA yupo, siyo lazima haya mambo utamke wewe!

WABUNGE FULANI: Sawa kabisa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Tuache. Yupo mzee wangu mmoja anasema kujimwambafai yaani uonekane wewe ni mwamba. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, nawaomba huko mlipo msiniharibie kazi yangu, mimi ndiye mwenye title ya utawala bora. Mimi ndio Waziri mwenye nafasi ya utawala bora, ukiendesha mambo kinyume na utawala bora unaniharibia kazi na sitaki Mheshimiwa Dkt. Magufuli anibadili. Mimi nataka Mheshimiwa Dkt. Magufuli aseme mzee endelea hapohapo ulipo. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, hili jambo humu ndani tumelizungumza na kwenye mafunzo tumelielekeza. Sasa nina hakika na upande mwingine pia mngepongeza maana ile vurumai siyo imepungua kidogo, imepungua sana, maji yametulia kwenye mtungi. Yametulia kwenye mtungi kwa sababu tumewapa elimu na wameelewa. Kwa hiyo, naunga mkono alichosema ndugu yangu Mheshimiwa Selasini kwamba tuwape elimu na tumewapa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie, mkitaka kujua kwamba masuala ya utawala bora nchi hii tunakwenda vizuri, mtupongeze tu. Jana, siyo juzi, Taasisi ya Transparency International inaonyesha kwamba mwaka 2017 duniani Tanzania tulikuwa wa 102 lakini jana tumekuwa wa 99. Kwa nchi zote duniani unazozijua wewe katika suala la utawala bora Tanzania ya 99. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachosikitika tu ni kwamba bado hatujamshinda Rwanda katika Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, yeye anaongoza sisi tunashika nafasi ya pili. Nasema kwa mwenendo huu tulipoacha kutianatiana ndani hovyo, nina uhakika tutakuwa wa kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo limegusiwa na wachangiaji ni Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini (TASAF) kutokufika baadhi ya maeneo. Nataka niwahakikishie TASAF tumefikia walengwa asilimia 70 nchi nzima, bado asilimia
30. Serikali imefanya maandalizi katikati ya mwaka huu malengo ni kufikia asilimia 30 iliyobaki. Kwa hiyo, wale ambao hamjafikiwa msiwe na wasiwasi, Serikali inafanya maandalizi ili tuweze kufikia maeneo yote.

Mheshimiwa Spika, lakini katika hili la TASAF nataka kutoa onyo moja, mnisikilize ili huko mliko msije mkaniletea matatizo katika Wizara yangu. Baadhi ya viongozi wa Wilaya wanawalazimisha walengwa wa TASAF kutoa michango bila kuwashirikisha na hasa ile ya bima ya afya. Tunasema zungumzeni nao wajiunge bima ya afya lakini wilaya moja tumeshamfukuza yule wa TASAF na mkubwa wake pengine anasubiri ngazi za juu huko. Michango ya maendeleo vijijini, sijui wanajenga shule, zahanati, watu wakiwa wagumu kuchanga wanakwenda kukata hela za TASAF, hilo ni marufuku. Nasema wilaya moja imeshatokea, taarifa zimefika kwangu, yule wa TASAF tumemfukuza, wale wengine wanasubiri wakubwa waliowaweka wawachukulie hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani mtu anapata Sh.20,000 kwa mwezi baada ya miezi miwili halafu wewe unamkata Sh.15,000 unasema mchango wa kujenga shule lakini wale ambao wana uwezo hawakuchanga, unakwenda kumchangisha maskini. Nasema ikitokea namna hiyo hatutavumilia. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, ilibaki pointi moja, walikuwa wanaomba wenzangu na mimi naomba hapohapo na kwa sababu unatupenda wote sawa utaniruhusu tu. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ndugu zangu, humu ndani nilitoa ufafanuzi nini maana ya barua kusema UFS, Kiswahili ni Kupitia Kwa, nikasema mtumishi yeyote wa Serikali ana haki ya kuwasiliana na mwajiri wake. Nikasema pia mtu akiandika barua ya kuomba uhamisho wewe Mkurugenzi, Mkuu wa Shirika, Katibu Mkuu anaandika barua inakwenda kwa mwajiri wake, anaomba barua ile ipite, wewe unachukua barua unaweka katika droo unasema mimi sipitishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilisema siku ile tukimpata kiongozi wa namna ile tutamuwajibisha. Anapopitisha barua kwako amekuheshimu, maana yake barua iende lakini with comments, anakupa fursa wewe kutoa maoni. Unaandika pale nakubali ahamishwe ili mradi nipate mbadala.

MBUNGE FULANI: Ndiyo.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Amekuja juzi hajamaliza miaka mitatu sipendekezi uhamisho huu. Barua lazima iende wenye kuamua kule kwamba uhamisho umekubaliwa au haukukubaliwa ni yule aliyemuandikia siyo wewe UFS. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini na watumishi nao nataka niwape darasa, barua yako ikishapitishwa haina maana kwamba uhamisho wako tayari umeshakubaliwa, ni kwamba pale imepitia inasubiri uamuzi kule juu. Niliomba siku ile msitufanyie kazi ya kuamua sisi tulioandikiwa barua, tuachieni sisi wenyewe tuamue. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono taarifa za Kamati hizi, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kushukuru kwa kupata nafasi hii ya kujibu hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezitoa pamoja na Kamati. Kama nilivyoshukuru kwenye hotuba yangu napenda kuwashukuru viongozi wa Taifa letu. Viongozi wa kitaifa wakiongozwa na Mheshimiwa Dkt. Magufuli Rais wetu, napenda kumshukuru Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti jinsi mnavyotuongoza humu ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niwashukuru sana Wabunge wote, kila mtu anajua kwamba, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora ni Wizara ambayo ina uzito wa pekee ni Wizara ambayo Wabunge nawapongeza wa CCM na wa Upinzani walipokuwa wanachangia humu ndani kila mmoja nilimwona ameweka mbele maslahi ya Taifa letu. Kwa hiyo, nataka niwashukuru sana na niwaahidi kuwa sitawaangusha katika majibu niliyowaandalieni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa nataka niseme, nchi yetu ipo salama wala haina matatizo ya kiusalama, kikubwa niseme vita dhidi ya rushwa katika nchi yetu ina mafanikio makubwa, wachunguzi wa ndani wanasema hivyo, wachunguzi wa nje wanasema hivyo. Vile vile kubwa zaidi mimi ndio Waziri wa Watumishi wa Nchi hii. Nataka nichukue nafasi hii kuwapongeza watumishi wa umma popote walipo, mtumishi yoyote awe kwenye shirika la Serikali, awe kwenye Wizara, awe kwenye Wakala ilimradi analipwa na Serikali Waziri wao ndio mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Watumishi wa Umma. Ukisikia tumenunua ndege za Serikali, ninyi ndio mmekushanya kodi, tumefanya nini, tumefanya nini, haya yote ni kwa sababu watumishi wa umma mmetekeleza wajibu wenu, huku nikizingatia wapo wachache wanaotuharibia sifa, lakini wengi mnafanya kazi nzuri na ndio maana mimi naona fahari ya kuwa Waziri wenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme jambo moja ambalo Waheshimiwa Wabunge walilizungumza hapa nisije nikalisahau, TASAF haijafika katika vijiji na shehia zote nchi zima. Kuanzia tarehe Mosi Julai tunajipanga tunataka tufike katika vijiji vyote, tunatakiwa tufike shehia zote bara na visiwani. Kwa hiyo hilo msiwe na wasiwasi, tulikuwa tunajipanga maana wanasema unajikuna pale unapofikia mkono, sasa mkono tumeurefusha. Hivyo, tuna uhakika tutakapoanza mwezi huo tutafanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichukue nafasi hii kuwashukuru Wabunge Wizara yangu imechangiwa humu ndani na Wabunge 85 orodha ninayo hapa, itaingia kwenye Hansard. Wizara yangu imechangiwa kwa maandishi na Wabunge 20, majina yenu ninayo hapa yataingia kwenye Hansard. Kama nilivyosema mambo yangu yapo mengi nikasema basi ngoja niende moja kwa moja kujibu hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamechangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Edwin Ngonyani anasema Serikali iangalie suala la watumishi wa afya walioajiriwa kihalali na Serikali kwa mkataba, lakini sasa wanaondoshwa. Maelezo yako hivi, Katibu Mkuu Kiongozi alitoa kibali kwamba watumishi wa afya wakati wa ajira badala ya kufuata mlolongo wa kawaida wa interview na kitu gani na kitu gani na kwa sababu walikuwa wanahitajika haraka akalegeza masharti kwamba badala ya kwenda kwenye Interview sasa waandikieni barua waende moja kwa moja wakaripoti kwenye maeneo ya kazi na ndivyo ilivyofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuajiriwa kwa mkataba kwa mtindo ule haikuwa sababu ya wewe kutohakikiwa kama wenzio. Kwa hiyo kwenye uhakiki wapo waliobainika pamoja na kwamba walikuja na vyeti vile hospitali, walibainika kwamba walikwenda kusoma lakini hawakuwa na elimu inayotakiwa kabla ya yeye kwenda kusoma. Hao ndio ambao baadaye waliondolewa, kwa nini? Kwa sababu walikwenda kusoma wakati hawana elimu inayotosheleza wao kwenda kusoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika masuala ya utawala bora, ndugu yangu hapa Msemaji wa Kambi ya Upinzani, hayupo lakini mtandao wake mkubwa ndugu yangu, yanga mwenzangu, alisema hivi kumeanza kujitokeza viashiri vya ubaguzi ndani nchi yetu kwa mitazamo ya itikadi ya vyama vya siasa, aidha viongozi wamekuwa wanavunja sheria kwa kutoa kauli na mtamko kinyume cha sheria. Maelezo ya Serikali yanasema hivi hakuna ushahidi uliowasilishwa kuona kuwa kuna hali ya ubaguzi kwa misingi iliyotajwa. Hata hivyo, kupitia Bunge hili naomba viongozi wa vyama vya siasa na sisi Waheshimiwa Wabunge wote tushirikiane kukemea matendo hayo yanapojitokeza. Watu wa upinzani wanataka amani, CCM wanataka amani, asiye na chama anataka amani.

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu, inapotokeza dalili kama hizo tushirikiane wote kukemea, kuna mtu mwingine akikemewa na CCM na ni wa CCM atasikiliza vizuri; kuna mtu mwingine wa upande mwingine akikemewa na Waziri wa Utumishi na Utawala Bora, anaweza asimsikilize vizuri, lakini akikemewa na Kiongozi na wa chama chake atasikia. Rai yangu wote tushirikiane linapotokea jambo kama hili wote kwa pamoja tulikemee, kila moja kwa nafasi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, amesema Msemaji wa Kambi ya Upinzani Tanzania imejitoa katika Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali Kwa Uwazi (Open Government Partnership) na akasema kwamba kujitoa kule kunaweza kukaathiri uendeshaji wa Serikali yetu kwa uwazi. Maelezo ya Serikali ni kwamba Open Government Partnership ilianzishwa na Rais wa Marekani Obama na Waziri Mkuu wa Uingereza, haikuwa katika nchi zote duniani, lakini sisi Afrika Tanzania tuna mpango unaofanana huu wa kuendesha Serikali kwa uwazi unaitwa African Peer Review Mechanism na tena juzi juzi hapa Tanzania sisi, Mtanzania Balozi Sefue amechaguliwa kuwa katika Bodi ya African Peer Review Mechanism mpango wa Afrika wa kujitathimini uendeshaji wa Serikali yao kwa uwazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukaona kwamba hizi kazi zinafanana, tukaona hakuna sababu ya kuwa katika hi na ile, lakini niseme tu kwamba hata wale ambao waliingia katika hiyo Open Government Partnership nchi zingine zimeshajitia kwa mfano Urusi imejitoa, Hungary imejitoa na nchi zingine zimejitoa. Kwa hivyo maelezo ni kwamba, sisi tuliingia kwa hiari, tumetoka kwa hiari yetu wenyewe baada ya kutosheka kwamba shughuli zile zinazofanywa na African Peer Review Mechanism, Mpango wa Afrika wa Kujitathimi wenyewe katika suala la utawala bora, tukaona inatosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimtoe hofu Mheshimiwa kwamba asiwe na wasiwasi Tanzania bado tunaendesha Serikali kwa uwazi na ukweli na ninataka niseme mfano ipo. Zamani tulikuwa tunaletewa hapa taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali, wanapelekewa Halmashauri, wanapelekewa Mawaziri wanaambiwa watekelezwe mle, lakini leo kila mwaka taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaletwa hadharani hapa Bungeni, inasomwa hapa Bungeni na inajadiliwa hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekaa kidogo muda mrefu katika Serikali nimewapoteza marafiki zangu wengi waliokuwa Mawaziri kutokana na ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu wa Serikali, ilijadiliwa hapa ndani Wabunge wakasema tunaomba mtupishe. Kwa hiyo hakuna mashaka juu ya Tanzania kuendesha Serikali kimya kimya, ingekuwa tunaendesha kimya kimya tusingeleta majadala kama huu ndani ya Bunge ukajadiliwa na kila mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna maoni ya Upinzani kwamba, kutokuwa na mifumo thabiti ya uratibu, ufuatiliaji na tathmini ya utendaji kazi wa kila siku ambao unatoa fursa kusomeka moja kwa moja kwenye kitengo kinachohusika na amesema hili Msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni. Maelezo ya Serikali ipo mifumo ya kielektoniki ya kukusanya mapato ya Serikali kutoka katika vyanzo mbalimbali kwenda Hazina moja kwa moja, mifumo hiyo ni pamoja na Government Electronic Payment Gateway, Local Government Revenue Collection Information System na malipo ya mshahara kwa njia ya mtandao Government Sales Payment Platform (GSPF).

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo napenda kuwaambia Waheshimiwa Wabunge kuwa, utaratibu wa kuratibu, kufuatilia na kutathmini mapato na matumizi ya Serikali kwa njia ya mtandao upo, unafanya kazi na baadaye kama nilivyosema humu ndani tuna mpango baadaye wa kubadili Wakala wa Serikali Mtandao kuufanya ni Mamlaka ya Serikali Mtandao ili tunapokuja katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali kama haya pasiwe na uhiari wa mtu kujiunga au kutojiunga ili mradi ni chombo cha Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine inasema matumizi sahihi ya dola’ kumekuwepo na matumizi mengi ya wananchi kupigwa, kujeruhiwa, kufariki kwenye vituo vya polisi ikiwa ni kubambikizwa kesi na kuwaweka mahabusu kwa makusudi hata kwa kesi zinazodhaminiwa. Maelezo ya Serikali vyombo vya dola vimekuwa vinatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa, aidha kuna mifumo mbalimbali iliyowekwa kwa ajili ya kuhakikisha vyombo hivyo vinatenda haki na pale panapokuwa na ukiukwaji wa sheria hatua huchukuliwa dhidi ya wanaohusika.

Mheshimiwa Naibu Spika, matukio ambayo yamebainishwa kwa mwananchi Musa Adam Said kubambikizwa kesi ya mauaji ni upungufu wa watendaji wachache tulionaona ambao wanatia doa Serikali yetu. Hata hivyo Mheshimiwa Rais ameelekeza wote waliohusika na tukio hilo wachukuliwe hatua kukomesha tabia hiyo na hatua zinaendelea kuchukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine inasema Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya wanapotumia mamlaka yao ya kuweka mtu mahabusu kwa saa 48 na 28, wazingatie Sheria za Tawala za Mikoa. Maelezo ya Serikali kama nilivyoeleza huko nyuma ni kweli Sheria ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ya mwaka 1997 inawapa mamlaka Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kumweka mtu ndani pale inapothibitika anahatarisha amani. Naomba Waheshimiwa Wabunge wanisikilize hii sheria inavyosema, nawaomba na huko walipo wanisikilize, mtu anawekwa ndani kama amehatarisha amani, sio watu wanadaiana madeni huko huyu hataki kunilipa, unampeleka kwa Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa unamweka ndani. Hawa wanadaiana, hawajahatarisha amani. Sasa hilo la kwanza, mtu asiwekwe mpaka awe amehatarisha amani, aidha Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya akitekeleza sheria kinyume na utaratibu anaweza akachukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na yeye mwenyewe kushtakiwa binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekemea hili jambo, tukakemea, tukakemea, Mwanasheria Mkuu wa Serikali hatamtetea mtu aliyevunja sheria makusudi kumweka mtu ndani bila sababu, Wazungu wanasema unlawful confinement umeshughulika na unlawful confinement, umetumia sheria hii vibaya utapelekwa mahakamani na huyo uliyemweka ndani na Mwanasheria Mkuu wa Serikali hatakuja kukutetea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali sisi tumeeleza kisiasa, Mwanasheria wa Serikali sasa ametoa waraka kwa wale wote waliopewa mamlaka ya kumweka mtu ndani, kila mmoja ana barua ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, nami amenipa nakala ninayo. Ikieleza ni mazingira yepi mtu anaweza kukwekwa ndani na ameeleza so emphatic, moja ujiridhishe kwamba ametenda kosa jinai; pili, uhakikishe kwamba asubuhi unaweka in writing, kwa nini unamweka ndani, nami nimesema humu ndani mara nyingi government moves on paper, hawa watu wengi wanaowekwa ndani ni kauli tu weka ndani, weka ndani. Ukimwambia hebu niandikie hawataki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo sheria inasema lazima wawekwe kwa maandishi; sheria inasema asubuhi yake afikishwe mahakamani, lakini lingine nataka nimalizie kuwaomba wenzangu wenye madaraka kama haya, utawala bora unasema kesi ikiwa mahakamani DC hasikilizi, Waziri hasikilizi, Waziri Mkuu hasikilizi, sheria inasema mahakama ya chini, uamuzi wake unaweza kutenguliwa na Mahakama ya juu. Wenzangu wengine wamejiingiza kwenye katika mambo ambayo tayari yalishahukumiwa mahakamani. Acheni, acheni acheni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine, je, Serikali huwa inafanya utafiti na kuangalia athari za maamuzi inayoyafanya? Maelezo hapa ni kwamba, Serikali inafanya tathmini kwa mfano, sisi katika Baraza la Mawaziri hatuamui kuna kikao cha wataalam wanakaa, kuna kikao cha Makatibu Wakuu wote, wao wanajadili mada ile, wanatoa ushauri, unaletwa kwenye Baraza la Mawaziri, Mawaziri tunafanya maamuzi baada ya kushauriwa na wataalam. Kwa hiyo niwatoe hofu ndugu yangu Mheshimiwa Msigwa Reverend hayupo hapa, amekosa uhondo wa majibu yake maana nilimwandalia yeye. Sisi hatufanyi maamuzi bila kutafakari, tunatafakari, tunashuriwa, lakini sio hivyo tu tunashaurika. Tukishauriwa na wataalamu ndio maana tunawasikiliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na tuhuma dhidi ya usalama wa Taifa, kuratibu na kuendesha vitendo vya utesaji wa raia wasio na hatia likitolewa mfano tukio la utekwaji wa mfanyabiashara maarufu Mohamed Dewji. Mwaka jana siku nahitimisha kama leo nilikuja hapa na Sheria ya Usalama wa Taifa, nikawasomeeni, jukumu la Usalama wa Taifa ni kukusanya habari na kuishauri Serikali full stop. Mtu ameuawa ni kesi ya polisi, mtu amepotea ni kesi ya polisi, mtu ametekwa ni kesi ya polisi. Kwa hiyo nasema, katika hili jambo tumekwishalieleza, wasiipake matope Idara yetu ya Usalama wa Taifa, hawa vijana wangu wanafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitoa mfano hapa siku moja, kiongozi wa upinzani, kiongozi wa kwenye upande wa pili wa chama cha upinzani, watu walipanga kumdhuru na wenyewe wanajua. Vijana wa Idara ya Usalama wa Taifa wakamfuata wakamwambia mzee tuondoke hapa, tuondoke hawa watu hawana nia nzuri na wewe, wakamtorosha. Sasa badala ya kuwapongeza watu wanaonusuru maisha ya mtu, ndio sasa tunawapakazia, Mohamed Dewj amepotea it is a police case. Sheria ya Usalama wa Taifa mnayo nendeni mkasome, kazi yake, ni kukusanya habari na kuishauri Serikali kwisha, kila nchi utakayokwenda, utaratibu ndio huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, iwe huru na kufanya kazi bila ya kuingiliwa na mamlaka yoyote. Jambo hili liko kwa mujibu wa kifungu cha 4 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Na.11 ya mwaka 2007. Lengo kuu ni kuhakikisha kunakuwa na ustawi wa utawala bora na kuondoa rushwa nchini. Ili kutekeleza jukumu hilo, kifungu cha 5 cha Sheria iliyotajwa hapo juu imebainisha wazi kuwa taasisi hiyo iko huru na haiingiliwi na mamlaka yoyote. Kwa hiyo, napenda kuunga mkono hapa matakwa ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwamba taasisi iwe huru na niseme kwamba hivyo ndivyo sheria inavyosema, pale mnapoona kwamba sheria imepotoshwa ni jukumu la Mtanzania na Mbunge yeyote kuiambia Serikali kwamba hapa mmepotoka na mimi kama Waziri mwenye dhamana ya chombo tutaunda Tume, tutafuatilia na kama ikibainika kinachosemwa kipo tutachukua hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, TAKUKURU kufanya kazi kwa hisia bila ya kuzingatia ushahidi dhidi ya watuhumiwa. Napenda niseme, kazi ya TAKUKURU ni kukamata na kupeleleza lakini anayefanya maamuzi Mahakamani siyo TAKUKURU. Kazi ya TAKUKURU ni kupeleleza na kupeleka mashauri Mahakamani mengine moja kwa moja, mengine kupitia kwa Mkurugenzi wa Mashtaka lakini anayeamua kwamba yule mtuhumiwa ana kosa au hana kosa ni Hakimu au Jaji anayesikiliza shauri hilo. Kwa hiyo, nafasi ya kumtia mtu hatiani TAKUKURU bila ushahidi haipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, watendaji wa TAKUKURU wasiteuliwe na Rais. Maelezo ya Serikali yako hivi, TAKUKURU wanafanya kazi kama jeshi, Rais wa nchi cheo chake kingine ni Amiri Jeshi Mkuu, watendaji wote wa vyombo vya ulinzi na usalama kwa mujibu wa sheria tulizojiwekea wanateuliwa na Rais. Endapo Bunge hili siku moja mtaamua kubadilisha sheria mkasema wawe wanateuliwa na Waziri wa Utawala Bora na ikipita mimi nitawateua. Mimi mtumishi wa Bwana, nitatenda kama Bwana anavyotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TAKUKURU itupie macho Idara ya Uhamiaji na Uwekezaji kwani zimegubikwa na rushwa na urasimu unaoathiri uwekezaji. Hoja hii imetolewa na Mbunge wa Liwale ndugu yangu Mheshimiwa Kuchauka. Sisi hapa tunasema tu kwamba taarifa tumeipokea, tutaifanyia kazi ili tujiridhishe kama yaliyosemwa ni kweli au hapana.

Mheshimiwa Naibu Spika, TAKUKURU imekuwa ikiwashtaki wafanyabiashara kwa kuwabadilishia makosa yanayohusu kiasi kidogo cha fedha na kuyafanya makosa ya uhujumu uchumi. Sisi hapa tumeeleza kwamba kwa mujibu wa aya ya 21 Jedwali la Kwanza la Sheria ya Uhujumu Uchumi ya 1984 makosa yote yanayoainishwa kwenye Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa isipokuwa tu kwa kifungu 15 ni makosa ya uhujumu uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu watuhumiwa kushtakiwa kwa makosa ya utakatishaji fedha ni vyema ikafahamika kuwa kifungu cha 3 cha Sheria inayokataza kutakatisha fedha Na.12/2006 kosa la rushwa ni mojawapo ya makosa yanayosababisha mtumishi kushtakiwa kwa kosa la utakatishaji fedha. Kwa hiyo, wanashtakiwa kwa mujibu wa sheria tuliyonayo. Inaweza kubadilika mpaka hapo Bunge hili litakapoamua kufanya mabadiliko. Kwa msingi huo, watuhumiwa hushtakiwa kwa makosa ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ilisema watendaji TAKUKURU wasiteuliwa na Rais. Hili nimekwishaliezea kwamba yeye ndiyo Amiri Jeshi wao Mkuu ndiye anayeteua wakuu wote wa vyombo vya ulinzi na usalama.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ni ya ndugu yangu Mheshimiwa Zitto, kwa nini fedha kwa ajili ya uendeshaji wa TAKUKURU hazikaguliwi na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wakati kila mwaka wanatengewa mabilioni ya fedha na Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007 inataka wakaguliwe. Kwanza, ndugu yangu Mheshimiwa Zitto, nakupongeza siku hizi umepata wanachama wapya wengi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo hapa ndugu yangu Mheshimiwa Zitto ni kwamba fedha zinazopokelewa kwa ajili ya utendaji wa majukumu ya TAKUKURU zinajadiliwa na Bunge lako Tukufu kupitia Fungu 30 ambalo hukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Kwa hiyo, nikutoe mashaka ndugu yangu kwamba fedha zao zinakaguliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ilikuwa kwamba Wabunge wanatunga sheria ambapo zingine zinanyima haki, kuna watu wanasingiziwa kesi za money laundering. Maelezo ya Serikali hapa yanasema TAKUKURU haina mamlaka ya kisheria kuzungumzia shauri lolote ambalo liko Mahakamani. Kwa hiyo, katika suala hili hatuna maelezo zaidi ya hapo kwa sababu jambo hili lipo Mahakamani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na swali kuhusu Sekretarieti ya Maadili linasema Serikali iingize katika mtaala elimu ya maadili katika shule na vyuo ili kuwajenga watoto wetu katika masuala ya maadili na utawala bora. Suala hili limetoka kwenye Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge ya Utawala Bora na Serikali za Mitaa. Maelezo ya Serikali ni kwamba mtaala wa elimu kuhusu maadili kwa shule za msingi upo na ulianza kutumika kuanzia mwaka 2017. Kwa hiyo, kwa upande wa elimu ya msingi mtaala upo na wanaendelea kufundishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika shule za sekondari mada kuhusu maadili imejumuishwa katika somo linaloitwa general studies, zamani tukiita uraia. Hata hivyo, tumeupokea ushauri wa Kamati kwamba tuendelee kuzungumza na Wizara ya Elimu ili sasa na vyuo vikuu navyo wapate masomo haya yanayohusu uadilifu, maadili na kupambana na rushwa wanapokuwa vyuo vikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine iliyoletwa inahusu Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), inasema utambuzi wa walengwa katika maeneo ambayo ni asilimia 30 ya vijiji, mitaa shehia nchini ufanywe mapema. Maelezo ya Serikali tunasema, utambuzi wa walengwa katika maeneo ambayo hayajafikiwa katika sehemu ya kwanza ya Mpango wa Maendeleo wa Kunusuru Kaya Maskini ambapo ni vijiji 5,693 utafanyika katika sehemu ya pili ya mpango inayotarajiwa kuanza 1 Julai, 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ni kuzifikia kaya maskini zote tulizonazo katika nchi hii. Kama nilivyoeleza pale mwanzoni wakati naanza kuongea kwamba tuna malengo kwamba Mbunge unapata tabu jimbo ni moja kuna vijiji wamo kwenye mpango vingine hawamo. Wewe Mbunge hawakuelewi na hata sisi Mawaziri tukienda mikoani hatueleweki, inaonekana kama kuna ubaguzi wa namna fulani lakini hoja ilikuwa ni masuala ya fedha. Sasa hivi kama nilivyosema tumejiandaa ikifika tarehe 1 Julai, 2019 tunataka tuwafikie walengwa wote ambao wanastahili kusaidiwa na mfuko huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilisema Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini unafadhiliwa na wadau wa maendeleo lakini hakuna nia ya dhati ya Serikali kusaidia kaya maskini kwa sababu kuna tofauti ya malipo kati ya walengwa waliopo Dar es Salaam na waliopo Kaliua. Jambo la kwanza nataka nilieleze Bunge lako Tukufu na sijui kwa nini hii habari imeenea hivi, fedha za TASAF ni za Serikali ya Tanzania, tumezikopa nje na zitalipwa na Serikali ya Tanzania. Kwa hiyo, maelezo kwamba TASAF inafadhiliwa na watu wa nchi za nje si kweli, fedha zile zitalipwa na Serikali yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango huu tulipouanza ziko nchi marafiki wakasema katika mambo Watanzania mnayoyafanya mojawapo zuri ni hili la kuhakikisha kila mtu anapata chakula, malazi, nyumba, sisi tutawaunga mkono. Kiwango walichokiunga huwezi hata mara moja ukalinganisha na kiwango ambacho Serikali yenu italipa. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge, wanufaika wa TASAF nje huko, Watanzania wenzangu wote muelewe kwamba fedha ya TASAF ni fedha inayotoka katika Serikali ya Tanzania inayoongozwa na Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Zitto alisema Serikali inaficha nini kutokana na uamuzi wa kuhamishwa Wakala wa Ndege za Serikali kutoka Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwenda Ofisi ya Rais, Ikulu tarehe 23 Aprili, 2018 kupitia Tangazo la Serikali alilolita. Majibu yake Mheshimiwa Zitto yako hivi, kwa mujibu wa sheria za nchi yetu anayegawa majukumu ya kila Wizara ni Mheshimiwa Rais na inasema Rais atapanga kazi hizo kwa Wizara mbalimbali kwa jinsi atakavyoona inafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, humu ndani hakuna Waziri aliyejipangia kazi za kufanya wote tumepangiwa na Rais. Hata hivyo, hii si mara ya kwanza, hili mbona ni jambo la kawaida. Kwa hiyo, kwa mujibu wa sheria za mgawanyo wa kazi hufanywa na Mheshimiwa Rais, sheria inasema as he may deem it fit, kwa jinsi atakavyoona yeye inafaa, siyo kwa jinsi atakavyoona Baraza la Mawaziri au jinsi atakavyoona baada ya kukaa na Abrahman na Mussa, hapana, kwa jinsi atakavyoona inafaa, nani, Rais. Ndiyo madaraka aliyotumia Rais kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka niseme hajafanya hivyo kwetu, kwa mfano, Tanzania Investment Centre imehamishwa kutoka Wizara ya Viwanda, Biashana na Uwekezaji imepelekwa Ofisi ya Waziri Mkuu, haikutokea hoja, limeonekana ni jambo la kawaida tu. Basi vilevile ilivyohama Tanzania Investment Centre kutoka Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kupelekwa Ofisi ya Waziri Mkuu ndivyo alivyofanya kwa Wakala wa Ndege za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sitaki kufafanua zaidi nisije nikaharibu lakini nataka niseme hao Air Tanzania mnaotaka wakabidhiwe ndege zote nane leo leo ndiyo wametufikisha hapa nchi hii ikawa haina ndege. Sasa tumejikusuru tumenunua ndege nane, walewale ambao tayari walishatufilisi si lazima tuwe tunawaangalia kabla hatujawakabidhi kila kitu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana Shirika la Ndege la Tanzania hizi ndege inazikodi kutoka Wakala wa Ndege za Serikali na tuna-monitor kila mwezi kuhakikisha wanalipa hela. Kwa sababu shirika lile likifilisika tena Serikali yenu ndiyo itabeba lawama hapa, mlitafuta hela, mkanunua ndege, mkawapa wabadhirifu walewale, limefilisika tena, mimi nitakuwa mgeni wa nani tena Air Tanzania ikifilisika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana tunasimamia ili kuhakikisha kwamba tunakwenda vizuri kibiashara na ili tusilalamike tena kwa sababu watu wengi wamefurahi sana. Nilikwenda kwenu kule ndugu yangu Mheshimiwa Zitto kutembelea Kasulu na sehemu nyingine kwa kutumia ndege hizi mpya. Miaka ya nyuma kabla ya hapo nilikuwa nakwenda na gari, mara ya mwisho nilipokuwa Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa nilikwenda kwa gari nikitokea Dodoma mpaka Kaliua, ukitoka Kaliua pale pori fulani hivi mnapita, ukiharibikiwa na gari ni wewe na Mungu wako. Juzi naambiwa Mheshimiwa Waziri kwa niaba ya Shirika la Ndege la Tanzania, safari yetu kwenda Kigoma itatuchukua muda wa saa mbili, nikapewa na peremende na soda, baada ya saa mbili niko Kigoma. Mwenyewe Mheshimiwa Zitto huyu wala haji kwa gari siku hizi, wapongeze Air Tanzania. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja kuhusu Wizara yangu ni nyingi sana, nisingependa kupoteza muda wenu, tumeandaa majibu yote, tukishamaliza kikao hiki cha Bunge tutatengeneza kitabu, tulichagua tu maeneo fulani tuyasemee lakini kwa yale maeneo ambayo mmeona hatukusema siyo kwamba hatuna majibu, majibu tunayo tutayaweka katika kitabu na tutawapatia. Nataka nichukue nafasi hii tena kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa ushirikiano mliotupa Wizara yetu. Tumeweza kufanya haya kwa sababu Kamati yetu ya Utawala na Serikali za Mitaa ililiomba Bunge litupitishie makisio, mkatupitishia na leo tumekuja hapa kuomba mtuwezeshe tena ili tuweze kutekeleza majukumu tuliyokabidhiwa na Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE.KAPT.MST. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwakunipa nafasi, nitangulie kusema kwamba, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kupongeza sana kazi nzuri inayofanywa na majeshi yetu. Kazi nzuri inayofanywa na askari waliopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, bila wao hapa Tanzania pasingekalika, wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe pole kwa ndugu zangu wa Rufiji, Kibiti, wajukuu zangu kwa mikasa wanayopata, wanauawa bila sababu, lakini kama mlivyosikia Jeshi la Polisi liko pamoja na ninyi jambo hili la muda litazimwa na majeshi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitoe pole kwandugu wanaohusika na msiba wa jana kule Arusha, niseme jambo moja, mchangiaji mwenzetu mmoja hapa asubuhi alisema kwamba itakuwa vizuri kama kila Mbunge akaonja jela, ili kuweza kujua mambo ya kule ndani. Nataka nimjibu kwamba Wabunge wa Tanzania ni waadilifu sana, tunajitahidi kila tunavyoweza ili tusiende jela na kwa sababu tulimpata mtu kaenda jela katusimulia, imetosha. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nijikite katika Jeshi la Zimamoto. Kwamba, Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Jeshi la Zimamoto kama Jeshi bado ni change, ilikuwa ni Idara chini ya Jeshi la Polisi lakini baada ya kufanywa kuwa Jeshi la Zimamoto na Ukoaji, Wizara mnatakiwa mlilee Jeshi la Zimamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivi kwa sababu gani mimi ni Mjumbe ya Kamati ya Ulinzi na Usalama. Nilipotembea Majeshi ya Zimamoto tumegundua matatizo mengi. Kwa mfano, iko Tume ya Majeshi inayopandisha vyeo, kuajiri ni Tume ya Majeshi, Magereza wamo, Polisi wamo, bado hamjawaweka Zimamoto. Sasa kama hawamo kwenye Tume watapandaje vyeo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kule Zimamoto ukimwondoa Thobias Andengenya ambaye ni Kamishna Jenerali wanaomsaidia wote acting,hizo bado tangu lilipoanza Jeshi pale mpaka leo wana act? Hii inawezekana kwa sababu Tume ya kuwapandisha haipo. Natoa kutoa rai watu wale hatua ichukuliwe haraka, tuwe na Makamishna siyo acting. (Makofi)

Suala lingine kuonesha kwamba sisi Wajumbe tuna mashaka kwamba pengine Waziri jicho haliangalii sana Jeshi hilo, asubuhi umetueleza hapa majengo mapya ya Polisi, Uhamiaji, Magereza, tukawa tunasubiri Zimamoto kimya, hata hela kumalizia Zimamoto ambayo tayari wameanza kujenga kule Dar es Salaam, kimya! Niishie hapo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nizungumzie juu ya magereza. Leo bajeti ya magereza ni kubwa kwa sababu Magereza hawajitoshelezi kwa chakula. Tumetembelea kambi za magereza nyingi tu. Tumekwenda Songwe tumeona ardhi nzuri, eneo nzuri la kulima, walituambia tunaomba Waheshimiwa Wabunge iambieni Serikali itupe matrekta, itupe vifaa vya kilimo, tuna uwezo wa kulima na kugawa chakula kwa magereza mengine, badala ya kuomba hapa Mheshimiwa Waziri hela ya magereza ya chakula omba matrekta wale watu wako tayari kujilisha wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni maeneo ya utawala. Leo Wilaya mpya zote zina matatizo ya kiutawala, kwa sababu hawana magereza hawana vituo vya polisi, hawana mahakama. Kwa hiyo, kuna kazi kubwa sana inafanywa na magereza kubeba askari kutoka Wilaya mpya kuwapeleka Wilaya mama watuhumiwa kwenda kusikiliza kesi, gharama ile ya mafuta ni kubwa. Ushauri wangu ni kwamba maeneo mapya ya utawala yanapoanza izingatiwe kwanza magereza, kituo cha polisi, mahakama ni sehemu ya utawala. Mkuu wa Wilaya hawezi kukamilika kama hana kituo cha polisi, kama hana magereza, kama hana mahakama…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE.KAPT. MST. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nilidhani dakika zangu ni kumi kumbe tano. Naunga mkono hoja kwa kuombatu kwamba Uhamiaji wajenge kituo cha uhamiaji kule Newala na mmalizie kituo cha polisi ambacho mnasema kimefika asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. KEPT. MST. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mtwara haujafanya vizuri mitihani ya darasa la saba hata kidato cha pili. Moja kati ya sababu zilizotufikisha hapo ni uhaba wa walimu, Mkoa una upungufu wa walimu kwa asilimia 40. Baadhi ya shule za msingi zina walimu watatu wakati madarasa ni saba.

Je, watafundishaje? Tunaomba Wizara inapoajiri walimu izingatie kuwa Mkoa wa Mtwara una upungufu mkubwa hivyo wapewe walimu wengi ili walingane na mikoa mingine.

Suala la pili ni vuguvugu la kufuta ujinga wa kutojua kusoma na kuandika limepungua sana. Waratibu wa Elimu Kata zamani walikuwa wasaidizi wa EWW. Idadi ya wananchi wasiojua kusoma na kuandika inaongezeka mwaka hadi mwaka, Wizara ifufue na iweke mkakati wa kufufua EWW. Waratibu wa Elimu Kata hawana kazi nyingi wapewe jukumu la kusimamia EWW kama ilivyokuwa hapo zamani.

Tatu, hali ya taaluma katika shule za msingi na sekondari hairidhishi na hii inasababishwa na shule zetu kutokaguliwa, wakaguzi hawatoshi na hawana usafiri. Serikali iongeze idadi ya wakaguzi na wapewe usafiri wa uhakika ili waweze kukagua shule zao zote. Naunga mkono suala la kuifanya Idara ya Ukaguzi kuwa Wakala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi hii kuchangia hoja hii muhimu sana ya Wizara hii ambayo ni uhai wa Taifa letu. Nataka nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa jinsi anavyowezesha Jeshi la Polisi kutekeleza kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza mdogo wangu Mheshimiwa Kangi Lugola anavyotekeleza majukumu yake kama Waziri wa Mambo ya Ndani. Pia nataka niwapongeze watumishi wote wa Wizara ya Mambo ya Ndani, kuna majeshi ya kila aina katika Wizara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, nataka kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Jeshi la Polisi katika nchi hii. Nitatoa mifano ya namna gani Jeshi la Polisi limetunusuru katika majanga ambayo tulikuwa nayo katika nchi hii. Tabia ya binadamu ni kusahau, ndiyo maana kila siku tunakwenda Msikitini, tunakwenda Kanisani kukumbushwa mambo. Siyo kama hatujayasikia, lakini kwa sababu tunasahau, ndiyo maana tumepangiwa kila Jumapili na kila Ijumaa twende kusali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mbunge, natoka Mtwara. Ili utoke Mtwara kwenda Dar es Salaam lazima upite Ikwiriri – Kibiti. Tulivamiwa Kibiti - Ikwiriri na watu ambao hatuwajui. Watu wengi wameuawa, usiku kulikuwa hakupitiki, Jeshi la Polisi limepambana, Kibiti kumetulia, Ikwiriri kumetulia, sisi watu tunaotoka Kusini tunapita Ikwiriri - Kibiti hata saa nane usiku, hakuna tatizo. Kazi hiyo imefanywa na Jeshi la Polisi.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, katika nchi yetu hii kuna mapori makubwa yaliyopo katikati ya Mji na Mji; Kasulu, Kibondo, mabasi yakitembea hasa giza likiingia lazima Askari wa Polisi wa-patrol kuhakikisha kwamba tunakuwa salama. Wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu, wale ambao wanabeza kazi ya Polisi, kaa, tafakari, hebu jiulize itokee siku moja Jiji la Dar es Salaam halina Mapolisi kwa muda wa nusu saa, hakuna Mapolisi wa kuongoza Traffic Dar es Salaam, badala ya kuwa traffic jam itakuwa imesimama kabisa. Polisi wanafanya kazi nzuri. Polisi wamepunguza ajali katika nchi hii. Ajali zimepungua, Mapolisi wanafanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwa umri wangu, jana nimeumia sana kuona kwamba watu wanasimama hakuna hata ile shukrani. Halafu jambo lingine nimelishangaa kwa utu uzima wangu, watu wameuliza maswali juu ya raia waliokufa ambao hawajulikani waliko; lakini hakuna aliyesimama anasikitika Mapolisi waliouawa wakiwa kazini wakifanya kazi ya kututetea sisi. Kwa mwendo huu mnataka kuwafanya vijana wakati mwingine sasa waseme eeh, kumbe ukienda Jeshi la Polisi wewe ni target? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Askari wetu wengi wamepoteza maisha, siyo kwamba walikuwa wanalinda shamba la baba yao; siyo kwamba walikuwa wanalinda duka lao; walikuwa wanatulinda sisi Watanzania wote bila kubagua wewe umetoka Mtwara, umetoka Lindi, umetoka Kilimanjaro, umetoka Kigoma nakadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema, mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. Nchi hii bila Polisi; hapa tu jioni magari yajae, maana yake leo watakuwepo watu kumpongeza Mheshimiwa Waziri kama atapita na Inshallah atapita. Magari yatajaa hapa. Ili tutoke hapa, bado mnataka Askari Polisi kutuondoa tu hapa Ukumbini. Je, Dar es Salaam! Kwa hiyo, nasema Traffic wanafanya kazi nzuri, mimi nimesimama hapa kuwapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Polisi hawa wanaitwa Askari wa Usalama wa Raia. Usalama wa Raia maana yake wanaangalia usalama wetu sisi. Sasa jana hapa palikuwa na hotuba za lawama tele, Polisi hawafanyi hiki, fulani amepotea hatujui aliko; sijui imekuwaje! Polisi anafanya kazi ya kulinda nchi hii kwa kusaidiwa kupewa taarifa na raia wema ili wafuatilie waweze kubaini ni watu gani wanauchafua usalama wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku tunaambiwa na tumepewa namba kwamba bwana una jambo la kuwataarifu Polisi? Piga hiyo namba. Hupigi namba; tangu mwaka 2018 tumemaliza bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani, watu wamekaa kimya, hawana mawasiliano na Polisi, hawajawapa taarifa ya Polisi, wanasubiri leo hotuba ya Mheshimiwa Kangi Lugola, waseme tena fulani hatumwoni na fulani ilikuwa hivi; na fulani. Umewapa taarifa Polisi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi Polisi walivyo wachache, sisi Watanzania tuliobaki milioni 55 ondoa hiyo idadi ya Polisi ambayo ni ndogo sana ukilinganisha na hao milioni 55, watawezaje kupata taarifa kama sisi wakereketwa wa nchi hii, wenye uchungu wa nchi hii hatuwapi taarifa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachotaka kusisitiza hapa, tuwape taarifa ya ushirikiano Jeshi la Polisi. Polisi pekee hawawezi kufanya yote ya kulinda usalama wa nchi yetu kama sisi hatutawapa taarifa. Kuja hapa na kutoa tu hotuba fulani hatumwoni, fulani kaibiwa, fulani imekuwa hivi, umewapa taarifa Polisi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi sitaki malumbano, nimesimama hapa kueleza kwamba tuna haja ya kushirikiana na Jeshi la Polisi ili nchi yetu izidi kuwa nchi ya amani na usalama. Siyo vizuri kutoa tuhuma humu dani bila kuwapa taarifa Jeshi la Polisi ili waweze kufanya uchunguzi, waweze kufuatilia kwa sababu Polisi kwa kawaida yao, wamesomea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu nataka kuzungumza habari ya utawala bora, imegusiwa hapa na pale. Ndugu zangu na Watanzania huko mliko, niwatoe hofu Watanzania wenzangu, Tanzania tuko salama. Nchi yetu, vyombo vya usalama vimedhibiti. Niambieni Afrika Mashariki yote hii leo, nchi gani watu wakipata matatizo ya vita kwao, wakipata civil war, wapi wanakimbilia kama siyo Tanzania? Hivi Tanzania pangekuwa mahali pa vurugu mechi wangekimbilia? Wanakimbilia Tanzania kwa sababu ni nchi ambayo ina amani, tuko shwari, vyombo vyetu vinafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana juzi niliumia hapa, mmoja akataka mjadala, tumjadili CDF kasema hivi. CDF kasema tu jamani eeh, sisi tutawafuatilia wakorofi wote, tukiwapata, tutawashughulikia. Hivi Askari kazi yake nini? Si kughulikia maadui wa nchi? Ukaja mjadala humu, CDF tumjadili; mnajadili nini? Askari tunapoapishwa na Rais, tunakula kiapo cha kulinda nchi yetu. Alichosema yeye na wanajeshi wenzake, wataendelea kulinda nchi yetu ili isichezewe. Ikawa nongwa. Unakuja mjadala humu! He! Freedom ya kukaa tunamjadili CDF aliyesema kwamba tutashughulika na wote wanaoleta chokochoko katika nchi yetu! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimalizie, maana dakika kumi naona ni chache. Upande wa utawala bora, nataka kuzitoa takwimu hizi; Watanzania tuna tabia ya kubenza mafanikio yetu. Tuko tayari kusifu mambo ya wenzetu lakini yetu hatusifu. Ndiyo maana hata humu ndani hata wenzangu wale wenye interest za mpira, ukimwambia panga timu ya mpira wa Ureno, atamweka goalkeeper, yote iko kichwani; lakini mwambie Taifa Stars juzi walicheza nani na nani? Hajui. Ndiyo tulivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka niseme upande wa utawala bora; na hapa uniruhusu kusoma. Nataka kusema, kwa utawala bora sisi katika nchi za Afrika tunang’ara. Maana mengi yaliyokuwa yanazungumzwa hapa ni ya kubeza utawala bora uliopo katika nchi hii. Kiashiria cha transparence International, hili ni NGO moja ya ki-International, inaeleza habari ya utawala bora dunia mzima. Wanasema kwamba Tanzania tunafanya vizuri. Tumepanda katika utawala bora, tulikuwa nafasi ya 193, sasa tuko nafasi ya 99, wanasema kwa utawala bora Tanzania iko juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako watu wa Afrobarometer hawa wanasema mwaka 2014 ilionesha kuwa asilimia 66 ya waliohojiwa walisema kuwa kiwango cha rushwa kimeongezeka; mwaka 2017 wakasema kiwango cha rushwa kimepungua, watu asilimia 85; TWAWEZA wakasema Tanzania utawala bora umeongezeka, rushwa imepunguza. Wale REPOA wakasema hivyo hivyo. Tungeweza kutoa mifano mingi sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKTI: Nimekuongezea dadika tatu.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa huruma yako. Kwa hiyo, ninachotaka kusema ndugu zangu, Watanzania tujivunie mafanikio tuliyonayo. Tanzania kama isingelikuwa nchi ya amani, mbona tuna wakimbizi hapa? Wamekimbia kwao. Mbona hawajakimbilia nchi fulani, mbona hawajakimbilia na nchi fulani na nchi fulani? Wamekimbilia Tanzania kwa sababu hapa wakija hakuna ile unamwona tu fulani, kabila gani huyuo ua! Kabila gani huyo, ua! Utawala bora nchi hii uko juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na matatizo hapa ya mauaji ya Albino, tumepambana, nchi imetulia; mambo hayo bado wapo mmoja mmoja, lakini na hao mipango tumeiweka kwa usalama wa nchi hii, hatutaki mtu auawe tu kwa sababu ni kilema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naunga mkono hoja. Nawaomba Wabunge wenzangu, mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni, Polisi wanafanya kazi nchi hii. Polisi na vyombo vyote vya usalama vinafanya kazi nchi hii, ndiyo maana ukipewa fursa ya kuongea, unaongea jinsi unavyotaka. Nchi nyingine wanavyoongea baadhi ya watu hapa, ilikuwa ukitoka tu hapa tayari anakusubiri pale uende ukakae ndani huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa watu mnaongea huru hapa, mnaongea mambo mengine ya ajabu ajabu, Mheshimiwa Rais ananunua vitu, amekuwa yeye ndiyo mnunuzi. Mmeambiwa hapa, Mheshimiwa Rais hajaenda shopping hata siku moja kwa ndege za Serikali, wala kwa jambo lolote la Serikali, vitu vyote vimenunuliwa kwa taratibu za manunuzi ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kushukuru kunipa nafasi kwanza nieleze naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nichukue nafasi hii kukupongeza sana Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Wajumbe wa Kamati kwa jinsi wanavyotuongoza vizuri yale mazuri mliyoyaona katika taarifa tumeyatekeleza kutokana na mwongozo na maelekezo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda umekuwa mchache nitagusia mambo matatu manne kwa kifupi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza limezungumzwa humu ndani nadhani katika Kamati zote nyingi suala la uhaba wa Watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwamba Serikali tumejipanga mwaka huu tunaajiri Watumishi 43,000 wa Kada mbalimbali lakini niungane na Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ndugu yangu Kandege kuungana naye nami niwahakikishie Watanzania wote ambao wameshiriki kwa mikono yao kujenga Hospitali 67, Vituo vya Afya 350, Zahanati kemkem kwamba hayatakuwa majengo ya maonesho tutaajiri Watumishi na tumekaa pamoja na Wizara ya Afya tumekaa na wataalam mbalimbali kuhusu suala la kuagiza vifaa tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwahakikishieni kwamba watumishi wataajiriwa na kama mlivyosikia wengine wamekwisha anza kuajiriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo limezungumzwa humu ndani kwa kirefu ni Mradi wa kunusuru Kaya maskini TASAF, TASAF tulikuwa tuna tatizo moja kwamba katika Vijiji tulivyokwenda tumefikia asilimia 70 ya walengwa katika vijiji vyote nchini tulifikia vijiji asilimia 70 na shehia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo tulikuwa tuna changamoto ya kumaliza walengwa waliobaki ambao hatujawafikia, nataka niwaambie Watanzania kwamba Serikali ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli imefanya maandalizi tumepata fedha za kutosha mwisho wa mwezi huu tutafanya maandalizi kabambe ya kuzindua TASAF Awamu nyingine ambayo tutamaliza thelathini wote waliobaki tutafika Vijiji vyote asilimia 100 tutafika walengwa wote asilimia 100 ili kuweza kuwahudumia wale ambao bado hawajafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Watanzania wenzangu kwamba sisi katika kijiji wasimamizi wa TASAF hatuendi na orodha ya walengwa. Walengwa wanapatikana pale kijijini ninawaomba tu wanakijiji wote tushirikiane katika kuwatambua walengwa wale ambao kwa uhakika tunajua huyu anahitaji msaada. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye Kijiji tukaambiwa kuna walengwa ambao hawakustahili kuwemo kwa kweli wa kulaumiwa ni Wanakijiji wenyewe kwa sababu wao ndiyo wanaoandaa orodha ya walengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imeshauriwa hapa tufanye malipo ki-electronic, tumejaribu kufanya majaribio mahali. Nataka niseme kwamba tutafika mahala tutafanya malipo kwa mtandao, lakini itawezekana tu kwa wale ambao wana simu na wanajua kusoma na kuandika. Kwa wale ambao itashinikana hivyo, sisi tutaendelea kuwafuata na kuwagawia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine lililozungumzwa hapa ndani ni suala la MKURABITA, naungana na Kamati. Kamati inasema tuwawezeshe zaidi, sisi tunakubali kwamba tuwawezeshe zaidi. Tukiwawezesha, naamini watafanya kazi nzuri zaidi. Ilitolewa hoja kwa baadhi ya Wabunge kwamba pengine mabenki yanakataa. Juzi kama alivyosema somo yangu Mheshimiwa George pale, nilikuwa Mpwapwa, tumekwenda kugawa vyeti. Bahati nzuri walialikwa mabenki yote pale, yapo manne pale Mpwapwa. Benki zote nne pale Mpwapwa zimetoa mikopo kwa watu waliokuwa wanamiliki hati za kimila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mabenki hayana matatizo. Nataka niseme, mahali popote ambapo mabenki yatawaletea matatizo labda hawawakopeshi kupitia MKURABITA, basi tupate taarifa katika Wizara na sisi tutachukua hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, hapa ndani asubuhi, mchana huu naona kumetulia kidogo, limezungumzwa sana suala la utawala bora. Nitakuwa sifanyi haki kama ni Waziri wa Utawala Bora halafu nisiseme jambo, tena kwa takwimu ili wale waliosema uongo waone haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utawala bora katika nchi, maana yake ni watu kuzingatia sheria, taratibu na kanuni ambazo zimepitishwa democratically. Democratically maana yake sheria imepitishwa na watu walio wengi. Humu ndani hata kama jambo hulitaki, lakini walio wengi wamelipitisha, hiyo ni sheria halali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia nzima kwa watu walioenda shule wanajua kwamba katika demokrasia walio wengi wape, lakini wale wachache uwasikilize. Kusikilizwa mnasikilizwa, si ndiyo maana mpo humu ndani! Si mpo wachache! (Makofi)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hata tusioenda shule tunalitambua hilo.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mtu mzima, naona aibu kusimama mwongozo, mwongozo! Hivi mtu anachangia, alikuwa anachangia mtu fulani asubuhi, hoja inapigwa pale, wanapiga kelele wee, mtu asisikilizwe. Kupiga kelele humu ndani wakati mwenzio anaongea huo ni ushamba. Huo ni ushamba! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie Watanzania wenzangu, nchi hii inaendeshwa kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni na imemweka Waziri maalum wa kusimamia utawala bora.

MBUNGE FULANI: Ambaye ni wewe.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Ambaye ni mimi. Kumbe unajua eeh!

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka niteo mifano hapa. Unajua Baba wa Taifa alipokuwepo aliruhusu column moja katika gazeti la Daily News ilikuwa inasema: “What They Say About Us?” Wanatusemaje walio nje kule? Kwa sababu wengine humu ndani mnapenda sana ku-quote mambo ya nje, sasa nami mzee nataka ku-quote huko huko mlikoenda nyie, niwaonyesheni kwamba ninyi hayo mnayoyasema siyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika kuhitimisha Hoja ya Kamati iliyowekwa Mezani nimeeleza suala utawala bora, nataka nieleze jinsi tulivyo, tunavyopiga hatua katika utawala bora. (Makofi)

(i) Kutokana na takwimu zinazotokana na tafiti, Tanzania imeonekana kuongeza kiwango cha utawala bora na hasa eneo la mapambano dhidi ya rushwa na hasa eneo la kutumia vizuri rasilimali za wananchi, na kodi ya wananchi. Sasa watu wamelipa kodi, hela inatumika vizuri wewe unataka nini zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti uliofanywa Transparency International; hawa wanazungumza mambo ya uwazi Kimataifa, wanaheshimika Afrika nzima, siyo Tanzania, hapana dunia nzima. Wanasema, 2019 kwa taarifa iliyotolewa na Transparency International, Global Corruption Parameter Africa 2016: “Tanzania imefanya vizuri zaidi kwa kupata alama 37 na kushika nafasi ya 96 katika nchi 180 duniani.” Lililopimwa ikiwa ni ongozeko la nafasi 21. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani Mheshimiwa Dkt. Magufuli baada ya kuingia madarakani, tunavyofanya vizuri katika utawala bora, Transparency International wamempandisha nafasi 21. Tumsikilize nani, Transparency International au wewe uliyefanya utafiti kwenye kijiji? (Makofi/Kicheko/Vigelele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuendelee. Kwa matokeo ya takwimu za utafiti wa kila mwaka, Tanzania imekuwa inapanda nafasi tangu mwaka 2015 Mheshimiwa Dkt. Magufuli anapoingia madarakani. Mwaka 2018 Tanzania ilipata alama 36 na kushika nafasi ya 99 ikilinganishwa na mwaka 2017 ambapo ilipata alama 36 na kushika nafasi ya 103. Kila mwaka tunapanda, tunapanda, tunapanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Utawala Bora anawaahidi kwamba tunataka siku moja Tanzania tuwe na digit moja tu, siyo kumi na ngapi, hapana. Kumi kushuka chini. Hivi mnayoyaona tunayoyafanya, mwendo ni huo wa kufika huko kwenye digit moja, hiyo ndiyo Tanzania ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli. Hiyo ndiyo Tanzania inayopendwa na watu wa nchi wa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende na matokeo ya kitakwimu hayo hayo na kama mtu anabisha aje nimwoneshe. Katika matokeo, takwimu hizo kwa upande wa Afrika Mashariki, Tanzania ni ya pili kwa Utawala Bora. Tunachuana sisi na Rwanda. Hivyo ndivyo wanavyosema wasomi na watu wenye authority katika mambo haya. Wewe unatuletea figure za ajabu ajabu hapa, ulifanyia wapi utafiti? Mao Tse Tung anasema: “no research, no right to speak. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaendelea. Kwa mujibu wa ripoti ya shirikisho Shirika la Mo Ibrahim Award, yule anayetoa zawadi kwa Marais katika masuala ya utawala bora, ambapo hutolewa ripoti yake kuhusu utawala bora kwa nchi za Afrika; mwaka 2018 Tanzania ilipata alama 58.5 kwa 100. Amevuka huyo! Ilikuwa nchi ya 14 katika Bara la Afrika katika suala la utawala bora ambapo ukilinganisha na huko nyuma tulikuwa na alama 57. Hao ndio wasomi, authority katika mambo ya utawala bora, nami wananisomesha wao. Kama mimi wananisomesha wao; je, wewe! (Makofi/Vigelele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende sasa; mimi nitakwenda nje na ndani, lakini nazungumza na watu wenye authority tu, wale ambao hawana authority sikuwa-quote hapa. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti mwingine wa taasisi ya ndani ya nchi wanaita Repoa. Mwaka 2017 imeonyesha wananchi saba kati 10 ya waliohojiwa walisema ushiriki wa Serikali katika mapambano dhini ya rushwa ni mzuri sana. Imani hiyo imeongezeka imetoka sasa 37% kwenye matokeo yaliyotolewa ukilinganisha 2018. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameulizwa wenye nchi yao, mnasemaje kuhusu habari ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli na Serikali yake na kwa habari ya utawala bora? Wakasema Serikali yake inafanya vizuri sana, sana. Wameulizwa mmoja mmoja; matajiri wameulizwa, masikini wameulizwa, CHADEMA wameulizwa, CUF wameulizwa, sembuse CCM; nao wameulizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tukija hapa, tunapongea watoto wetu wanatusikiliza huko nje; na watoto wa siku hizi shomile, wamesoma, analinganisha alichosoma yeye kwenye kitabu cha watu wenye authority anakulinganisa na unayosema wewe. Hivi ukifika nyumbani siyo ajabu akakwambia eeh, baba, mama ulisoma kitabu gani? Kitabu hiki hapa, kisome.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya sababu kubwa ya mafanikio ya haya ni utashi wa kisiasa (political will). Ili nchi ipambane na rushwa, lazima kuwe na ipambane na political will. Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Magufuli ana political will ya kupambana na ufisadi. Alisema ataanzisha Mahakama ya Mafisadi na ameianzisha. (Makofi)

Mheshiiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka nimalizie point moja, mbili za mwisho, maana darasa hili huwa linawapotea, hamlipati kila siku. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na utashi huo, imani ya wananchi imeongezeka, nidhamu ya watumishi wa Umma ninaowaongoza mimi Serikalini imeongezeka, imeimarika. Matumizi mabovu ya fedha za ndani, ndani ya Serikali yamedhibitiwa. Kwa sababu tunakusanya vizuri mapato, tunadhibiti matumizi mazuri na watalaam wanasema tunazitumia fedha zetu, ndiyo maana tukienda huku ndege huuuuu, mpaka Songea kwa watani zangu amalo ilikuwa ndege hazitui, zinaenda. Mtwara huko sisemi, Mwanza na kwingineko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi namsikiliza Rais wangu, amewaulizeni wala hamjamjibu bado. Kwa nini Mheshimiwa Dkt. Magufuli unanunua ndege kwa fedha taslimu? Akawaambieni kama hela ninayo mfukoni kwa nini nikope? Hivi mtu anayekopa si hana kitu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Tusikilizane. Mifumo ya utendaji kazi imeimarishwa ikiwa ni pamoja na kuziimalisha taasisi simamizi ikiwemo Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa. Tulikuwa na Wilaya…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua ndivyo walivyo, wala hatuwashangai, ndivyo walivyo. Mimi Waziri nimepewa muda wa kutosha.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mkuchika, naomba umalizie endelea.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa hilo neno la mwisho “endelea”, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema hivi, tumepandisha vyombo vya kupambana na rushwa. Tulikuwa na Wilaya 21 hazina ofisi, tumefungua ofisi, tumewapa na magari. Mwaka huu Wilaya zote nchi hii kila Wilaya ina Ofisi ya TAKUKURU. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nimewasikiliza sana asubuhi. Vyama vingi tangu vimeanza nchi hii, hoja ni Katiba mpya, Katiba mpya. CCM tukasema haya, tukaja humu ndani kutengeneza Katiba mpya. Tulipopiga kura Serikali tatu au ziwe mbili? Walio wengi wakasema ziwe mbili. Kitu gani kingine? Hawakupata walichotoka. Hivi humu ndani aliyechukua mpira akaweka kwapani tukasababisha Katiba mpya isipatikane, ni CCM au nani? Sasa leo bila aibu mnasimama hapa, tunataka Katiba mpya, Katiba mpya, aliyekimbia na mpira, mpira ukavunjika alikuwa nani? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naona ndugu zangu wamefurahi, wameelewa. Wale ambao hawakuelewa, wameelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi/Kicheko/Vigelele)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji
MHE. KEPT. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Napenda kuchukua nafasi hii kwanza kumpongeza Rais wetu John Pombe Magufuli anavyoiendesha nchi hii. Wapo ndugu zetu walikuwa wanapiga kelele za ufisadi, ufisadi, amewafungulia Mahakama ya Ufisadi. Wale waliokuwa wanasema kwamba huyu fulani fisadi wamewachukua, tuleteeni kwenye Mahakama ya Ufisadi tuwashughulikie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua nafasi hii kuunga mkono hoja ya Wizara ya Maji. Nataka niwakumbushe Wabunge wenzangu Kanuni zetu zinasema Kamati Ndogo ya Bunge ya Kudumu inapofanya kazi ni sawasawa na Spika amekaa anaendesha Bunge. Bajeti tuliyoletewa hapa imefanyiwa kazi na wenzetu wa Kamati inayohusika na suala la maji. Kwa hiyo, unapokuja hapa tu ghafla bin vuu ukasema tufumue, turudishe, tufanyeje, mbona mnawadharau Wajumbe wenzetu wa Kamati waliofanya kazi hii?

Mimi naungana na wenzangu wanaosema tutafute namna ya kuboresha Mfuko wa Maji, yale mawazo yanakaribishwa, lakini wewe unasema tufumue, tuikatae, darasa hilo sisi wanafunzi tunalikataa, darasa la kukataa bajeti sisi tunalikataa, bajeti hii itapita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nataka nianze kwa kuwapongeza wapigakura wangu wa Jimbo la Newala. Kule kwetu Newala tuna ustaarabu wa kuvuna maji ya mvua, kila nyumba ya bati utakayoona ina kisima kimechimbwa na kwa sababu kule kwetu water table iko very low tunachimba mpaka futi 14, tunajenga kwa zege, tunajenga kwa tofali, tunakinga maji ya mvua ya kutosha familiaile mwaka mzima. Ndiyo maana hali ya maji Newala unafuu upo kidogo, si kwa sababu ya maji ya bomba ya Serikali, hapana, tunakinga maji ya mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tusingekinga maji ya mvua hali yetu ingekuwa mbaya sana. Nataka nitoe mfano na hili mimi nataka niiseme Serikali yangu, mnapofanya vizuri nawapongeza, mnapoharibu nawasema. Hivi mradi wa maji wa Makonde kwa muda wa miezi miwili mmewakatia umeme, watu wa Newala tupate wapi maji ya bomba ya kunywa?

Nimeambiwa umeme juzi umerudi, naomba jambo hili lisirudiwe tena. Mheshimiwa Rais aliposema kata umeme amewahimiza Maafisa wa Serikali mnaotakiwa kulipa maana yake mlipe kwa wakati siyo mnazembea kulipa halafu wanakwenda kuadhibiwa wananchi ambao kila mwezi mkiwapelekea ankara wanalipa. (Makofi)

MHE. KEPT. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa pili ule hata ukawaelimishe namna gani, huyo anayeongea…
Mheshimiwa Naibu Spika, huyo anayeongea alituhamasisha humu tuikatae bajeti, mimi sikukubaliana naye lakini nilikaa kimya, ndiyo ustaarabu wa humu ndani. Ndiyo maana tunawaambia nchi hii CCM itatawala ninyi mtabaki tu kama mnyama fulani anaona mkono wa binadamu unatembea anasema unadondoka kesho, unadondoka kesho, ndiyo mlivyo, tunakamata Serikali kesho, kesho, kama mwendo wenu ni huo hampati kushika nchi hii. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nataka wale ambao hamuifahamu Newala, Waziri anaifahamu, Naibu Waziri anaifahamu, sisi tunaishi mahali kunaitwa Makonde Plateau. Wale wanaokumbuka geography Makonde Plateau definition yake wanasema a raised flat piece of land (kipande cha ardhi kilichonyanyuka), ukiwa kwenye plateau maana yake umekaa kwenye meza, ndivyo ilivyo Newala na Tandahimba. Tuko juu kwa hiyo water table iko chini sana, hakuna mahali tunapoweza kuchimba tukapata maji na ndiyo maana tunategemea sana maji ya bomba na ndiyo maana kwenye miaka ya 1950 watu wa Newala wenyewe tukaanzisha Kampuni inaitwa Makonde Water Corporation, tukakopa hela Uingereza tukaanzisha mradi wa maji Makonde, tukawa tunauza maji, tunatengeneza pesa, watu wanapata maji ya kunywa. Serikali baada ya uhuru ikatuhurumia, ikauchukua ule mradi ikaufanya mradi wa maji wa kitaifa. Nakuomba ndugu yangu Wenje, aah nakuombandugu yangu Lwenge… (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu Wabunge ni yale yale ya kutokujua, mimi nilidhani upande wa pili wanaelewa kwamba ulimi hauna mfupa kumbe hawajui. Mimi nimewasamehe maana tumefundishwa, baba uwasamehe maana hawajui watendalo, mimi nimewasamehe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni ile ya Makondeko ilichukuliwa na Serikali, ukafanywa ndiyo mradi mkubwa wa kitaifa. Mheshimiwa Naibu Waziri, mradi wetu ule wa kitaifa unasuasua kwa sababu upatikanaji wa maji siyo mzuri, miundombinu imechakaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu upande wa Wizara yale mambo ambayo nilitaka kuyamalizia nitawaandikia, mimi naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. KAPT. (MST). GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, upatikanaji wa maji mradi wa maji Makonde hauridhishi. Tunapata maji ya bomba chini ya asilimia 30 ambayo ni kidogo sana ukilinganisha kitaifa. Moja, booster station ya kati ya Mkunya na Makote ilijengwa tangu 2006 lakini haijakamilika na haijakabidhiwa, kwa nini hawaifanyii kazi? Serikali ieleze mradi huu utakamilika na kukabidhiwa lini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbili, mabomba na mitambo ya Mradi wa Maji Makonde yamechakaa. Chanzo cha Mkunya kinatakiwa kuwa na pump tatu lakini iko moja tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, chanzo cha Mitema kinahitaji pump sita ila ziko mbili tu. Mradi uliagizwa kutangaza tenda ya kubadilisha mabomba kwa shilingi bilioni mbili, mkandarasi alipatikana lakini fedha hazikutumwa. Serikali inunue kwanza pump na iharakishe upatikanaji wa mkopo kutoka India, ulioahidiwa, ili mradi uweze kukarabatiwa na kuongeza upatikanaji wa maji. Msimu wa mvua kwetu umekwisha wasio na visima hawawezi tena kukinga maji ya mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, skimu ya umwagiliaji ya Chikwedu – Chipamanda. Tumeelezwa mkataba bado kwa sababu taratibu za manunuzi zimechelewa Ofisi ya Mkurugenzi wa Wilaya. Hili halikubaliki, halmashauri isimamiwe skimu iweze kukamilishwa tuweze kuendeleza kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, Wilaya ya Newala ilikuwa na mradi mdogo wa maji – Luchemo. Mradi huu ulikumbwa na mafuriko mwaka 1990 hivyo ukafa. Wizara haijachukua hatua za kuufufua. Nashauri mradi huu ujengwe upya maana wananchi waliokuwa wanategemea mradi huo sasa hawapati maji safi ya bomba.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama kueleza hoja moja tu, baadhi ya watu mmezungumza juu ya utendaji kazi wa Idara ya Usalama wa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme kama ifuatavyo, ukijua kazi inayofanywa na Idara ya Usalama wa Taifa yale mliyoyazungumza humu ndani msingeyazungumza, ninayo sheria hapa ya Usalama wa Taifa ya mwaka 1996 nataka nikusomeeni kwa mujibu iliyopitishwa na Bunge, nataka nikusomeeni kazi za Idara ya Usalama wa Taifa, ukizisikiliza hayo yote mliyoyasema hayahusiani na Idara, fulani kapotea police case, fulani kaumizwa police case, haihusiani na Idara ya Usalama wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kifupi kazi ya Idara ya Usalama nchi yoyote ni kutafuta habari na kuishauri Serikali.

Nasema imeandikwa kiingereza Mimi nitasema kwa Kiswahili kwa sababu ili Watanzania wanaosikia waliopo hapa wote tupate uelewa mmoja kifupi ninachotaka kusema hoja mlizozitoa kuhusu Idara hazihusiani na Idara, hoja mlizozitoa kuhusu Idara haishauri Serikali mambo ya uchumi, haifanyi nini, haifanyi nini hamna ushahidi, katika nchi zote duniani Idara ya Usalama inatafuta habari nakuishauri Serikali yake kimya kimya (Makofi).

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana hakuna nchi utasikia msemaji wa Idara ya Usalama wa Taifa kasema hili, kasema hili, hakuna kitu kama hicho, kwa hiyo unaposema Serikali hawakuishauri unao ushahidi?

Sasa Sheria inasema hivi; “Subject to the control of the Minister the functions of the service shall be” shughuli zimewekwa nne;

(a) to obtain, correlate, and evaluate intelligence relevant to security (kukusanya habari, kutafuta habari na kuzifanyia tathimini) wanapofanya hayo hawayafanyi kwenye mkutano wa hadhara.

(b) To cooperate as far as practicable and necessary with such other organs of state (kushirikiana na vyombo vingine vya Idara zinazoshughulikia na usalama wa nchi), mna ushahidi hawana ushirikiania nao.

La tatu, linasema; to advise Ministers, where the Director-General is satisfied that it is necessary to do so (kuwashauri Mawaziri, kuishauri Serikali).

La nne, inasema to inform the President, and any other person or authority which the Minister may so direct, of any new area of potential espionage, sabotage, terrorism or subversion. Haya yote haya mambo ya kuhujumu uchumi ya nini, nini yanafanywa kimya kimya hakuna nchi inaita mkutano wa hadhara na kusema jamani tumevamiwa, hakuna nchi inaita mkutano wa hadhara na kusema tumefanya hivi, tumefanya hivi ninaomba Waheshimiwa Wabunge...

Mdogo wangu Zitto nakuheshimu sana, nimepewa mimi nafasi ya kuongea, ulipewa nafasi ya kuongea, hivi kwa nini mna-disturb wenzenu wakisema.

Sasa kwa sababu ya dakika tano nataka nifunge pia kwa haya maneno yamo ndani ya sheria inasema hivi; “It shall not be a function of the service (haitakuwa shughuli ya Idara ya TISS) (a) to enforce measures for security; mambo ya mabavu mabavu kushika, kumkamata huyu haitakuwa kazi yake. (Makofi)

(b) Inasema; to institute..., sikilizeni nikupeni darasa.(Makofi)

(b) Inasema haitakuwa shughuli ya Idara to institute surveillance of any person or category of persons by reason only of his or their involvement in lawful protest, haitakuwa kazi ya Idara ya Usalama wa Taifa kumchunga chunga mtu, kumfuata fuata imo ndani ya sheria. (Makofi).

Kwa hiyo, kifupi ninachotaka kusema ndugu zangu, tukitaka kusema mambo mazuri yanafanywa na Idara hii mashahidi ninyi mimi nataka kutoa mfano, palikuwa na kilio mahala palikuwa kuna msiba, watu waliofiwa wamenuna, wakataka kumpiga kiongozi wa chama, wakamwambia wewe ndiye umesababisha mtu wetu afe, alitoroshwa na watu wa Idara ya Usalama nini hamjui? (Makofi/Kicheko)

Kwa hiyo, tatizo mkiambiwa yale mnayoyajua yanayowauma mnapiga kelele.

Mheshimiwa Naibu Spika, Nakushukuru.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dokta John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua anazochukua kukabiliana na Upotevu wa Mapato ya Serikali katika Sekta ya Madini
MHE. CAPT. GEORGE H. MKUCHIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa tena nafasi. Mimi leo nimefarijika sana katika Bunge hili. Watu wote waliochangia upande wa CCM na upande mwingine hakuna aliyesema Rais kakosea. Hakuna aliyesema Rais kakosea, mwingine anasema hapana tunashangilia mapema mpira, tusubiri mwishoni. Mimi ninavyofahamu mpira unashezwa dakika 90, filimbi ikipigwa tu mwenye timu yake anashangilia hangoji dakika ya mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema kwa kifupi sana, ndugu yangu pale Mheshimiwa King ameunga mkono hoja tunashukuru, Mheshimiwa Mchengerwa ameunga mkono hoja tunashukuru, ndugu yangu Mheshimiwa Mtolea pale ndiyo yule kasema kwa nini tunapongezana bado safari ni ndefu (encouragement), watu wote wa Tanzania wanajua kwamba Rais anafanya kazi ngumu ili aendelee kuifanya ile kazi nzuri anahitaji kutiwa moyo, ndiyo hiki tunachokifanya hapa. Hata hivyo, nampongeza ndugu yangu Mheshimiwa Mtolea, wala hajasema Rais kakosea kuunda wala hajasema, ndiyo nilichompenda hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia anasema tuongeze nguvu za kuzuia dhahabu. Kwa upande mwingine ukilinganisha lugha yake hiyo ni kama vile yupo pamoja na Rais, hivi wenzangu mnaonaje? (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu Mheshimiwa Hasunga ameunga mkono hoja, lakini hili suala la mikataba mimi nilisikiliza juzi Rais wakati anapoongea, alisema yale mambo ya kisheria, pale ambapo mikataba haikukaa sawa, pale ambapo sheria haikukaa vizuri, Serikali itatuletea hapa Bungeni ili tuipitie na kurekebisha. Sasa naomba usitie unga kupika ugali kabla maji hayajachemka. Ukitia mapema utapata uji badala ya ugali. Tusubiri muda ukifika hiyo kazi tutaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu Mheshimiwa Kangi Lugola ameunga mkono, ndugu yangu Mheshimiwa Tundu Lissu pale alikuwa anacheka maana yeye pamoja na lugha yote ya ukali, hakuna Mheshimiwa Tundu Lissu aliposema napinga Rais kuunda Tume, mmemsikia anasema hivyo? Tuko naye pamoja katika hili. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua Bunge moja hapa aliwahi kuja Spika wa Bunge la Kenya anaitwa Ole Kaparo, akasema kwamba, katika nchi zingine vipo vyama vinaitwa Chama Pinga. Chama Pinga maana yake yeye hata ukimwambia mbili jumlisha mbili jawabu nne atakwambia hapana tano. Sasa sifikiri kama ndugu yangu Mheshimiwa Tundu Lissu amefika huko kwenye hatua ya kusema mbili jumlisha mbili saba. Kwa hiyo, nasema nimemsikiliza sana ndugu yangu Mheshimiwa Lissu yeye ni mzalendo na jana kwa mfano hata wenzetu upande wa Upinzani walisema,. tulikuwa tukipiga kelele hamkutusikia, hamkutusikia, sasa tumekusikieni leo, si mseme basi Alhamdulillah mmetusikia. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lile la kuwasifu Marais waliotangulia nadhani Mkuu wa Shughuli za Serikali Bungeni kasema, sisi ni Bunge la mwaka 2015-2020 tunashughulika na mambo yaliyomo ndani ya kipindi chetu. Wale Marais waliotangulia walianza Magufuli anaendeleza pale walipoachia wenzake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, kama nilivyosema sitaki kupoteza muda, hili Azimio limepokelewa vizuri, pande zote mbili wamelipamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naunga mkono hoja, pili nataka kueleza kwamba hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, Kamati inayosimamia Wizara hiyo pamoja na wachangiaji wengi wameelezea umuhimu wa kupatikana haraka iwezekanavyo watumishi wa Idara ya Afya. Wameeleza kuwepo kwa upungufu katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kutoa taarifa na kuwaondoa mashaka Waheshimiwa Wabunge kwamba kama mnavyokumbuka mwezi Oktoba, 2016 Serikali ilifanya zoezi la uhakiki, katika uhakiki ule walipatikana jumla watu 14,000 wa kada mbalimbali ambao waligundulika kujipatia kazi kwa vyeti vya kughushi. Kati yao walikuwemo watumishi 3,310 kutoka katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa uhakiki huo Serikali ilisitisha ajira kwa maana ya kujiridhisha tuna watumishi wangapi. Napenda niliarifu Bunge lako tukufu kwamba zoezi lile limekamilika na kazi ya kwanza iliyofanywa na Wizara yangu ilikuwa ni kuziba pengo la wale watu ambao walionekana wameondolewa katika utumishi wa umma. Kwa hiyo, ilitoa kibali kuajiri watumishi mbadala 2,500 ili kufidia upungufu uliotokana na watumishi wa kada ya afya kuondolewa; kwa hiyo hao zoezi hilo linaendelea. Pamoja na hayo katika mwaka wa fedha 2017/2018 kama mtakumbuka Bunge hili lilipitisha ajira ya watumishi 52,436 zikiwemo nafasi za ajira za watumishi wa kada ya afya 14,104 sawa na aslimia 26.9 ya nafasi zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hili zoezi la watu 52,000 tutakapokuwa tunaajiri asilimia 26 sawasawa na watu 14,000 watakuwa wametoka sekta ya afya. Pia katika bajeti mlionipitishia juzi, na ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge Serikali imetenga nafasi zingine za ajira 49,536. Ukichanganya wale 49,000 na 52,000 tutaajiri watumishi inafika karibu laki. Sasa ajira ya watumishi wa kada ya afya katika hao laki moja ni 16,205 sawa na asilimia 32.7 watakuwa ni watumishi wa sekta ya afya. Kwa hiyo utaona kwamba Serikali tumejipanga. Hata hivyo msisitizo wa Serikali kwa sasa ni kuhakikisha huduma za afya hazikwami kwa namna yoyote ile na hivyo ninawataka waajiri wote katika Serikali za mitaa kufanya uwahishaji wa matumizi kada za afya pamoja na kada nyingine kwa kuwatoa watumishi wa kada hizi sehemu mbalimbali ambapo wapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nataka kusisitiza watu wengi, Waheshimiwa Wabunge wengi walipokuwa wanachangia hapa ndani walikuwa wanaeleza kwamba ziko zahanati zimefungwa, kuna vituo vya afya vimefungwa kwa kukosa watumishi. Mimi nataka kuliambia Bunge lako tukufu, nilishatoa maagizo na leo narudia tena, Serikali ya CCM haitoruhusu kituo cha afya kifungwe kwa sababu ya kukosa watumishi. Nilishasema ikitokezea mahala pengine amefariki maana si lazima iwe kwa sababu ya kufukuzwa, iwe kwa sababu yoyote ile Serikali ya CCM haitaruhusu kituo cha afya kifungwe kwa sababu ya kukosa mtumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikipata taarifa katika Wizara yangu haraka haraka pale walipo wengi nitahamisha mtu nitapeleka wakati zoezi la kuajiri linaendelea naomba nilieleze Bunge lako Tukufu kuanzia leo yoyote ambaye aliongea humu ndani ambaye ana uhakika kuna zahanati haina mtumishi imefungwa; kuna kituo cha afya kimefungwa huduma zinakosekana niletewe taarifa hiyo wakati Bunge hili linaendelea nitapeleka watu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nitangulie kusema kuwa naunga mkono hoja hii na Mheshimiwa Waziri mimi Mbunge wa Newala Mjini watu wangu wamenituma nikuambie kwamba wanaridhishwa sana na utendaji kazi wa Wizara yako, wanapongeza sana mlivyopanua Kiuta sekondari sasa kuwa high school, ulivyosaidia kule Mnyambe na ulivyosaidia madarasa. Wananchi wanasema wataendelea kushirikiana na Serikali kutekeleza wajibu wao pale inapobidi nguvu za wananchi zinahitajika. Kwa sababu tunavyofahamu Serikali yetu haikuwahi kuahidi kwamba kila kitu kitatolewa bure, tunafanya ubia kati ya Serikali na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nataka niseme leo nimesoma press release ya Mbunge, namheshimu sana lakini mambo yaliyosemwa mle mengine wanasema ukikaa kimya, quietness means consent, ndiyo maana nimeamua nisikae kimya, nijibu hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja inayozungumzwa pale kwamba Mheshimiwa Rais aliahidi kuongeza mshahara mwaka huu.

Naomba mnisikilize, watu wazima wakikaa kwenye faragha wanasikilizana, mimi hamjaniona nawazomea hata siku moja. Mnasema mambo wakati mwingine yanaudhi lakini nakaa kimya, ndiyo nidhamu ya Bunge. Hivi mzee mzima na mvi kama hizi nianze kuzomea ooh, ooh, aah. Basi mna mtu wa kumuiga mfano mbona hamniigi mfano? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilikuwa Iringa, Mgeni Rasmi alikuwa Rais nimemsikiliza live, hayo mnayosema moja, maana unajua Kiswahili kigumu, inawezekana tukasikiliza wote wawili mimi nikaelewa vingine na wewe ukaelewa sivyo lakini kwa sababu ni mtaalam wa lugha ya Kiswahili nataka kusema alivyosema Rais jana. Amesema hivi, mwaka jana sikuahidi kupandisha mishahara. Akasema siku zote Serikali inapandisha mishahara kulingana na uwezo wa kifedha. Lingine akasema kupanga ni kuchagua, tuna shida ya kujenga reli, reli ile ya kwenda Kigoma zinaanguka kila siku tangu 1905 mpaka leo zaidi ya miaka 100, tunajenga reli ya kisasa, tumenunua ndege, hauwezi ukaleta watalii kutoka nje unawapeleka Ngorongoro unataka wapande ndege nazo za nje, domestic flights.

Mheshimiwa Mwenyekiti, akasema nawaomba Watanzania wenzangu tuchape kazi. Waliopo mashambani waongeze uzalishaji kama mimi mkulima wa korosho, mliopo ofisini mchape kazi na mliopo viwandani muongeze uzalishaji. Hali ya uchumi itakaporuhusu, maneno ya jana ya Rais na mimi nilikuwa pale futi moja kutoka kwake, sasa ooh nilisikia, nilisikia, mimi nilikuwa futi moja pale ubavuni kwake, akasema hali ya uchumi itakaporuhusu nitapandisha mshahara tena sitangoja sikukuu ya May Day.

Sasa nikuambieni pale kupanga ni kuchagua, yeye akasema kwa ufahamu wake kupanga ni kuchagua, akasema ilibidi tuamue, je, tuongeze mishahara tubaki tulivyo na barabara mbovu, bila ndege, bila reli (standard gauge).

Kuzomea ndiyo tabia yenu lakini hakuachi mimi kusema. Mimi siwezi kuacha kusema kwamba kuna watu wameamua ku-behave kana kwamba wako sokoni, mimi nitasema tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, akasema hali ya uchumi itakaporuhusu nitapandisha mshahara, sitangoja May Day, nikiambiwa tu mahesabu kule Hazina yamekubali siku hiyo hiyo napandisha, ndivyo alivyosema. Kupanga ni kuchagua, akasema ilibidi tuamue, je, tutekeleze haya kwanza au tugawane hela kwa kuongeza viwango vya mishahara. Leo mtu anasimama hapa anasema Rais kasema uongo, mwaka jana alituahidi, mwenyewe amekanusha hakusema, msimtie maneno mdomoni ambayo hakuyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena aliyetoa press aliwahi kufanya kazi utumishi, kuna mahali anasema watumishi sisi tunalipishwa…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Nasoma hapa ninyi, humu ndani unaruhusiwa kuwa na note book siyo kusoma risala, mimi naandika hapa point form, mimi ni mwalimu najua kuandika lesson notes, najua namna ya kujiandaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile press release inasema wafanyakazi wanalipishwa skills development levy, wrong. Skill development levy analipa mwajiri halipi mfanyakazi. Hivyo hayo maneno unategemea uyapate kwa mtu senior citizen, senior retired civil servant hajui kama skills development levy inalipwa na mwajiri na hawezi kwenda kufuta ile maana ameiandika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka niweke sawa hilo, sasa nataka nichangie upande wa ajira ya walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mtakavyokumbuka Oktoba, 2016 tulifanya zoezi la uhakiki wa watumishi. Katika uhakiki ule ilibainika baadhi yao walikuwa na utumishi hewa wakiwemo na walimu. Mara moja baada ya kuona idadi ya walimu imepungua kilichotokea ni kwamba Serikali imeajiri watumishi tayari…

KUHUSU UTARATIBU . . .

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa darasa ulilotoa. Unajua wakati mwingine unaweza ukaongea kwa jazba ukasahau hata ulichokuwa umekisema. Serikali inasimama hapa kujibu hoja za Wabunge. Hili ninalolisema mmelisema. Hivi mlitaka mkisema jambo la uwongo tukae kimya tu? Quietness means consent. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini dakika wanazoninyang’anya hizi utanifidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo imezungumzwa na pande zote mbili; upande wa upinzani na upande wa CCM ni suala la msingi la ajira kwa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ajira kwa walimu jana Mheshimiwa Rais alipohutubia kule Iringa aliwaambia wafanyakazi kwamba watumishi 22,150 wataajiriwa mara moja. Katika hao 7,000 sawa na asilimia 31.6 watakuwa ni walimu. Hii tunatekeleza bajeti ya mwaka huu tulio nao sasa na tutakapoanza mwaka mpya, juzi mmepitisha bajeti ya watu wengine 49,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka niseme kwamba hakuna mtu ndani ya Serikali anayependa pawe na uhaba wa walimu, kila jitihada zitafanyika. Kama nilivyosema kwa upande wa afya siku ile, nilisema kama kuna zahanati yoyote iliyofungwa kwa kukosa watumishi nileteeni, wako walioniletea tumeshafanya utaratibu tunawapeleka watu kwa sababu niliahidi hakuna zahanati itakayofungwa kwa kukosa watumishi. Nasema tena kwa upande wa elimu hapa nilipo mimi ndiyo Waziri wa Utumishi, hakuna shule itakayofungwa kwa kukosa walimu, unayo jimboni kwako nenda kaniletee tutafanya mpango kupeleka walimu mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nataka niseme kuna halmashauri nyingine walimu mnawarundika shule moja hasa shule za mjini. Tunaomba Waheshimiwa Wabunge wote hapa tushirikiane pale ambapo walimu wamezidi tuwapeleka sehemu ile ambako kuna shida ya watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilisimama hapa kuunga mkono hoja, haya niliyosema sijaogelea nje ya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najibu hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge wa pande zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nataka nianze kwa kuunga mkono hoja. Vile vile napenda kumpongeza Waziri wa Fedha kwamba baada ya kutoka Chuoni kufundisha akaja kwenye siasa. Hotuba aliyoitoa mwaka huu ya utangulizi wa Serikali hii imefanya nini, ameshahitimu siasa. Alimaliza kila kitu katika yale mambo kumi aliyoyasema yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, basi hotuba ya Waziri wa Fedha hakuna hotuba yako imenoga kama ya mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, upande wangu Utumishi na Utawala Bora kulikuwa na hoja kama tatu nitazieleza kwa kifupi. Kwanza ni suala la ajira, Wabunge wengi wamesimama wametaka kufahamu suala la ajira likoje. Nataka nieleze tu kwamba Serikali kwa makusudi ilisimamisha ajira kwa muda katika kipindi cha kuhakiki watumishi. Maana unaweza ukampa mtu promotion kumbe mfanyakazi yule fake, unaweza kumpa mtu promotion kumbe vyeti vyake sio halali. Ndio maana ikasimamishwa kwanza, ili zoezi la uhakiki likashakamilika zoezi lianze. Zoezi limekamilika, tumewabaini wafanyakazi hewa 19,708, tumewabaini vyeti fake 14,409, tazama pesa kiasi gani tumeokoa. Malengo ya uhakiki makubwa ni mawili:-

Mheshimiwa Spika, kwanza tuwapate watu wafanye kazi ambayo wanataaluma nayo. Mtu anaingia theatre anapasua watu awe ni mtu ambaye cheti chake kinamruhusu kupasua watu. Tumewabaini watu wanavaa majoho meupe wanaingia walikuwa wanafanya operation sasa hatuwezi kucheza na maisha ya watu. Ndio maana Serikali ikasema kwanza, tuwe na uhakika kila mmoja anafanya kazi ambayo ana taaluma nayo.

Mheshimiwa Spika, lakini lingine nalo Utawala Bora ni kusimamia rasilimali za umma zitumike vizuri. Unapowalipa wafanyakazi hewa, unapowalipa watu ambao vyeti vyake si sahihi, hayo ni matumizi mabaya ya fedha za umma. Kwa hiyo, nataka niseme baada ya hili zoezi kukamilika tumeshaanza ajira, mpaka Juni, tutakuwa tumeajiri watumishi 22,150 mpaka tarehe 30 ya mwezi huu.

Mheshimiwa Spika, katika hao Walimu ni 7000 tayari process ya ajira inaendelea na Afya 8000. Kwa hiyo, nataka niwaombe Wabunge wenzangu wale ambao tunasimamia ujenzi wa zahanati tusiwe na mashaka, tumalize zahanati hakuna zahanati itakayokamilika ikaacha kufanya kazi eti kwa sababu haina watumishi, tutawaajiri. Hilo ni la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, ilikuwa upande wa mishahara na hili limeongelewa na Mheshimiwa Masoud Abdallah Salim wa Mtambile, Mheshimiwa Susan Kiwanga wa Mlimba na Ndugu yangu Mheshimiwa Mwita Waitara. Kifupi walisema kwamba, watumishi wa umma hawajaongezewa mishahara kwa muda mrefu sasa na pia hata nyongeza yao ya mwaka (increment) hawapewi. Hali hii inasababisha wanapostaafu kupata mafao kidogo. Maelezo ya Serikali ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, si sahihi kwamba watumishi wa umma hawajaongezewa mishahara kwa muda mrefu kwani nyongeza hiyo haikutolewa kuanzia mwaka 2016/2017. Kama nilivyoeleza kutokana na uamuzi wa Serikali kupitia Muundo wake na kufanya zoezi la uhakiki watumishi. Aidha, hivi sasa Serikali inaboresha utoaji wa huduma ya elimu na afya na kutekeleza miradi maendeleo ambayo itakuwa chachu ya ukuaji wa uchumi na maendeleo kwa ujumla katika siku za baadaye.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uwezo wa kibajeti imekuwa vigumu kugharamia utoaji wa huduma ya elimu na afya, kutekeleza miradi hiyo mikubwa pamoja na kuongeza mishahara kwa wakati mmoja. Uwezo wa bajeti utakapokuwa mzuri Serikali itatoa nyongeza na mishahara kwa watumishi wake.

Mheshimiwa Spika, tulipokuwa Iringa kwenye Sikukuu ya Wafanyakazi, Mheshimiwa Rais alisema hali ya hewa, akiona kwamba hali ya hewa inaruhusu hatangoja kupandisha siku ya sikukuu, hata ngoja kupandisha siku ya mwaka mpya, muda wowote hali itakaporuhusu mishahara itapanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilitoa nyongeza ya mwaka Annual Salary Increment kwa watumishi wa umma na itaendelea kutoa nyongeza hiyo katika mwaka wa fedha 2018/2019 na miaka mingine kadri ya uwezo wa bajeti utakavyoruhusu.

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho lilihusu upandishaji vyeo. Hili lilitolewa na Mheshimiwa Sophia Mwakagenda na Mheshimiwa Dkt. Prudenciana Kikwembe. Hoja ilikuwa kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ilizuia stahiki mbalimbali watumishi ikiwemo upandishwaji madaraja kupisha zoezi la uhakiki. Kwa kuwa zoezi limekamilika watumishi wamepandishwa madaraja, kwa tarehe za sasa na sio kwa tarehe walizostahili kupanda madaraja. Hali hiyo inasababisha watumishi kustaafu na kupata mafao kidogo. Serikali iwalipe stahiki zao watumishi kwa vile zoezi la uhakiki limekamilika.

Mheshimiwa Spika, maelezo ya Serikali ni kweli Serikali ya Awamu ya Tano ilizuia stahiki mbalimbali za watumishi ikiwemo upandishaji madaraja ili kupisha zoezi la uhakiki ambalo lilifanyika kwa manufaa makubwa na kuokoa kiasi kikubwa cha fedha za Serikali kwa kuondoka watumishi hewa. kama nilivyosema 19,708, watumishi wenye vyeti fake 14,405. Hata hivyo kwa watumishi hata hivyo kwa watumishi ambao walikuwa na barua ya kupandishwa vyeo, mishahara yao iendelee kubadilishwa katika mifumo shirikishi na taarifa za kumbukumbu za watumishi kila mwezi kwa kuzingatia tarehe walizostahili kadri ya tarehe yao ya kustaafu kazi kwa umri ilivyokaribia.

Mheshimiwa Spika, iwapo kwa bahati mbaya yupo mstaafu ambaye alikuwa na bahati ya kupandishwa cheo lakini mshahara haujabadilika hadi alipostaafu; mstaafu wa namna hii anashauriwa aende kwa aliyekuwa mwajiri wake amjazie fomu maalum ya madai ya malimbikizo ya mishahara inaitwa Mheshimiwa Spika, Salary Arrears Claims Form ili aweze kulipwa madai yake kwa njia za hundi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, kama nilivyosema naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalam ya Walimu Tanzania wa Mwaka 2018
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, kwanza nianze kukushukuru kwa kunipatia nafasi hii, lakini nieleze kwamba mimi naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taaluma mimi ni mwalimu. Nilikuwa naona wivu sana wenzetu wa taaluma nyingine bodi kama hizi wanazo siku nyingi, tena wao wachache kuliko sisi walimu, ndiyo maana nikasema kwamba pengine hoja hii imechelewa, ndiyo maana nikasema ninaunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameeleza umuhimu wa kuwasajili walimu. Ndiyo maana nasema kama zoezi hili limechelewa, sio sisi wa mwanzo, Wakandarasi wanayo Bodi, Madaktari wanayo Bodi, Wauguzi wanayo Bodi, Wafamasia wanayo Bodi, sasa katika watumishi wa Serikali ambao mimi ndio Waziri wao, watumishi wengi wa Serikali ni walimu. Kwa hiyo, kukaa muda mrefu bila kuwa na chombo kama hiki, tumechelewa. Ndiyo maana nikasema mimi naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Mawaziri tunahudhuria Vikao vya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kuna jambo wanaita harmonization, wanataka muhtasari wa masomo yote katika nchi mbalimbali ufanane ili mwalimu aliyehitimu Rwanda aweze kufundisha nchi yoyote, lakini ili uweze kwenda kufundisha nchi nyingine lazima uwe umesajiliwa katika nchi yako. Leo sisi tunahitaji walimu wengi wa kwenda kufundisha Kiswahili nje, lakini kwa kukosekana hili huwezi ukatambua mwalimu gani ana sifa ya kufundisha Kiswahili nje ya nchi. Bodi ikishafanya kazi yake itakuwa ni muda muafaka sana wa kuweza kuwasajili ili waweze kutambulika kwa urahisi huko nchi za nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa imetolewa hoja ambayo siafikiani nayo kwamba muswada unakusudia kuwadhibiti walimu. Mimi nasema mtumishi yeyote wa umma aliyeajiriwa kuna kiwango cha kudhibiti ndiyo maana kunawekwa sheria, taratibu na kanuni, ile unamdhibiti mtumishi. Hata mtu binafsi akimwajiri mtu, yule aliyemwajiri anampa miiko ya ile kazi, sasa sembuse mwalimu!

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nataka kusema jamani, hakuna mtu muhimu katika historia yetu sisi wote kama mwalimu. Ndiyo maana wanasema mwalimu ndio mzazi wa pili, kwa nini? Mtoto akizaliwa, amekua, anapata malezi kwa baba na mama. Baada ya pale anamkabidhi yule mtoto kwa mwalimu, ndiyo maana mwalimu lazima awe ana nidhamu ili yule mtoto afuatishe nidhamu ya mwalimu. Ndiyo maana taaluma hii ya ualimu kweli kama bodi tunayoiunda itasaidia kudhibiti mwenendo na tabia ya walimu, mimi naunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kutoa mfano, mimi nimesoma Arusha, shule moja inaitwa Ilboru, nilikwenda pale form five na six. Nimekuta shuleni kuna kitu kinaitwa Ilboru Personality. Moja, marufuku kwenda mjini kununua karanga umevaa uniform ya shule unatafuna karanga huku unatembea. Ukifanya hivyo, wanafunzi wenzako wanakuchora, akikuona mwalimu anakuchora, Jumatatu unapewa adhabu na unatangazwa kwenye assembly kwamba huyu weekend hii aliharibu heshima ya Ilboru Personality. Alitafuna karanga barabarani akiwa anatembea, alinunua mahindi akawa anatembea barabarani. Pakawa pana nidhamu nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani sisi tuliosoma tulikuwa tunaangalia mwalimu amevaaje? Amenyooshaje nguo yake? Nguo yake ni nzuri kiasi gani? Kwa sababu mwalimu ni kioo cha mwanafunzi. Kwa hiyo, tusiwe na hofu hapa ya kusema kwamba watakuwa walimu wanadhibitiwa, hapana. Lengo ni kwamba tufanye kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naikubali sana hoja iliyotolewa hapa na ndugu yangu, Mheshimiwa Hongoli, anasema kwamba hatuwezi kukubali walimu wanavaa hovyo. Nimesema hapa, na mimi namuunga mkono. Mwalimu akivaa hovyo, mtoto naye atavaa hovyo.

Mimi nilikwenda kwenye sherehe moja, Siku ya Walimu Duniani, sitaki kusema ni mkoa gani au wilaya gani, nikawa mgeni rasmi. Yule waliyemleta kuja kusoma risala hakuchana nywele. Katika mazungumzo yake akasema;“Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya” maana nilikuwa Mkuu wa Wilaya. Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya, walimu tuna hali ngumu, mishahara midogo na nini na nini, wenzake wakampigia makofi ukumbi mzima. Mimi nikamuuliza, je, na kutochana nywele nako hapo, nayo ni hali ngumu ya uchumi? Mwalimu ana heshima yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mtaalam wa lugha. Nilifaulu somo linaitwa english literature, tukasoma mambo ya akina Shakespeare, nilipata one distinction, nilishinda kuliko watoto wa Malkia. Walimu wakaniambia niende nikasomee uanasheria, maana kweli ningeweza. Huku literature, huku history nikapata two, kiswahili nikapata three. Nilipokwenda Chuo Kikuu nikaambiwa wewe ni mtu wa sheria. Nilipomwambia baba yangu, akaniambia sitaki, nataka ufanye kazi ya heshima. Kazi gani? Ualimu. Nika-comply, nikaenda kusomea ualimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba bodi hii ambayo tumeiunda itasaidia sana kuinua kiwango cha utendaji kazi wa walimu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imetolewa hoja hapa; nataka nieleze tu jinsi walimu wanavyoshughulikia upande wa madai ya malimbikizo ya mishahara. Serikali imeweza kulipa jumla ya shilingi bilioni 45 kama malimbikizo ya mishahara ya kwa watumishi 27,437 baada ya kukamilika kwa zoezi la uhakiki wa watumishi hewa na vyeti vya watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika malipo hayo, jumla ya walimu 15,000 walilipwa jumla ya shilingi bilioni 16. Nataka niwahakikishie walimu, ni dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano kuhakikisha kwamba malimbikizo ya madai ya walimu yanakuwa historia na mwaka huu tutaendelea kumaliza matatizo yote yaliyobaki kwa madai ya walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa upandishwaji vyeo, nataka nieleze tu kwamba baada ya kukamilika kwa zoezi la uhakiki, jumla ya watumishi 44,275 wakiwemo walimu 28,000 wamepandishwa vyeo na taarifa zao kuidhinishwa kwenye Mfumo wa CHMIS kuanzia mwezi Novemba, 2017 hadi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa hapa juu ya uhaba wa walimu na mimi nakubali. Uhaba tulionao kwa watumishi, siyo walimu tu, katika fani nyingine zote, lakini tunachotaka kusema, tunapoajiri tunawapa walimu kipaumbele kwa umuhimu wao, ndiyo maana mmeona tumekuwa tunaajiri sana walimu wa masomo ya arts, baadae ilipoonekana wamekuwa wengi, wamepelekwa kwenda shule za msingi, lakini na juzi hapa tumeanza kuajiri walimu wa masomo ya sayansi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo hapa ni kwamba idadi ya walimu wa sayansi na walimu wa arts iwe sawa. Hakuna anayesema kwamba masomo ya arts ni muhimu kuliko sayansi wala sayansi muhimu kuliko arts kwa sababu yote hayo yanahitajika. Tunahitaji wanasheria na ma-engineer wote wanahitajika. Huwezi ukawa pande zote kama hujasoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kati ya nafasi za ajira mpya 52,436 kwa mwaka 2017/2018 kada ya elimu ilitengewa jumla ya nafasi 16,000 hadi sasa jumla ya walimu 6,840 wameshaajiriwa na kugawanywa kwenye vituo vyao mbalimbali. Katika mwaka wa fedha 2018 Serikali imepanga kuajiri watumishi 49,000 wakiwemo na kada ya ualimu. Kwa hiyo, ninachotaka kusema ni kwamba, tutakapokuwa tumetoa ajira kwa walimu kama tulivyokusudia tunaamini kwamba, uhaba wa walimu utapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ambayo yalikuwa yanahusu Wizara yangu, yaliyoguswa katika mjadala hapa ndani naona kama nimeyajibu. Nirudie kukushukuru tena kueleza kwamba, naunga mkono hoja, tuwape walimu hadhi yao kama tulivyowapa hadhi ma-engineer, tulivyowapa hadhi wanasheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.