Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula (32 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nami ni mara ya kwanza kuchangia hoja katika kipindi hiki cha bajeti, naomba pia nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuweza kunifanya niwepo hapa.
Pia nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Ilemela kwa imani yao kubwa ambapo walipata mateso kwa miaka mitano bila huduma kwa jamii, lakini wakaamua kuachana na hiyo na kurudisha Chama cha Mapinduzi kuweza kuongoza Jimbo lile. Nasema sitawaangusha, tuko pamoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniamini na kunipa dhamana hii kuweza kuwa msaidizi wake katika Serikali hii ya Awamu ya Tano. Nachukua fursa hii pia kupongeza na kuishukuru familia yangu hasa muwe wangu Julius Mabula, watoto kwa namna ambavyo wamekuwa wavumilivu kwa muda wote niko hapa; nawashukuru ndugu, jamaa na marafiki ambao wamekuwa karibu sana kuhakikisha kazi yangu ya uwakilishi inakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe pongezi sana kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya, Makamu wa Rais na hasa kwa kuwa ni mwana mama, Waziri Mkuu, Mawaziri na Manaibu Waziri, Wabunge wote lakini pongezi za dhati sana kwa Wizara husika ambayo leo tunajadili hoja yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie machache kuhusiana na Wizara yangu kama jinsi ambavyo yameguswa na wachangiaji wakati wakichangia hoja ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Nianze na migogoro. Naomba niseme wazi, migogoro ipo mingi, ndiyo maana Wizara imechukua hatua ya kupeleka waraka katika mikoa kuwataka waweze kuzungumzia migogoro iliyopo na chanzo chake ili tuweze kuona namna ya kuitatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke suala la migogoro ya ardhi ni suala mtambuka, haligusi Wizara moja, ndiyo maana limeingia sana katika mifugo na wakulima kule, lakini kwenye ardhi lipo, ukienda TAMISEMI lipo, ukiingia Maliasili na Utalii lipo, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) lipo. Kwa hiyo, suala hili kama Wizara tumeshaanza mchakato wa kukaa pamoja tuweze kulipitia kwa pamoja. Kwa hiyo, tukipata zile taarifa za mikoani, tutajua chanzo cha migogoro ni nini?
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ardhi imekuwa ni tatizo na ni chanzo kikubwa, basi tutajua. Inatokana na wananchi kuvamia maeneo? Inatokana na wakulima kukosa maeneo ya kutosha? Au inatokana na wafugaji pengine kutopata maeneo? Je, mazingira tunayalinda? Kwa hiyo, ili tuweze kupata ufumbuzi wa kweli ni lazima hizi Wizara zikae pamoja kama ambavyo tumekwishaanza tuweze kuona chanzo na namna bora ya kuweza kutatua. Kama ardhi imekuwa ni tatizo, pengine tuweze kuona namna ambavyo tunaweza kulitatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia mpango wa matumizi bora ya ardhi nao ni changamoto. Kwa hiyo, ni lazima pia tuangalie. Kuna wengine walitoa hoja kabla ya kilimo, suala la viongozi kupewa maeneo. Haikataliwi kama amefuata sheria, lakini suala la msingi ni je, sheria zimezingatiwa? Kwa hiyo, hapa tunasimamia ile Sheria ya Ardhi Namba (4) na Namba (5) ya mwaka 1999, kuona ni kweli limefuatwa. Kwa sababu kuna process ndefu ya kupata eneo. Lazima utapitia katika vikao husika. Vikao hivi kama vinakiukwa ndipo hapo ambapo unaona matatizo yanakuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wakati mwingine tamaa za viongozi katika maeneo ya chini kuweza kutaka kumilikisha watu kwa kukiuka taratibu. Pia na siasa inaingia. Tukiondoa siasa katika suala la umilikaji wa ardhi, migogoro ya wakulima na wafugaji, migogoro ya ardhi itapungua sana, kwa sababu kila mmoja anaguswa katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imezungumzia suala la kuwezesha vijana na sisi kama Wizara tunasema sawa. Wamezungumzia suala la kurejesha ardhi na kuwapa, lakini bado niseme Halmashauri zetu zitahusika sana kutambua yale maeneo na kuweza kujua ni jinsi gani vijana hawa tunawapa ili waweze kujikita katika uzalishaji ambao utakwenda vizuri katika kujipatia kipato.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala pia la wavuvi. Naomba ku-declare interest kwa sababu Jimbo ninalotoka ni la wavuvi. Kama Serikali ilivyozungumza, nami naomba, kwa sababu Sheria ya Uvuvi itakwenda kupitiwa upya, niwatake sana watu wa Jimbo langu na wale wote wanaotoka katika maeneo ya uvuvi waweze kuchangia mawazo yao ili sheria ile itakapokuwa imetoka, maoni yao yaweze kuwa yameingia. Walikuja kwa timu ya uongozi wakatoa kero zao nyingi, Waziri aliwapokea, tulikwenda nao na sisi tunasema kama Serikali tutayapitia haya kwa sababu kilio kinapotolewa ni lazima pia upitie, lakini nao wana sehemu kubwa ya kuchangia katika Muswada ule utakapokuwa umeanza mchakato wake, watoe mawazo yao ili tuweze kujua ni jinsi gani migogoro hii inakwisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, Upinzani wamezungumzia suala zima la Tume ile ya Bunge iliyoundwa katika kuchunguza migogoro na wakataka kujua ni maazimio mangapi yametekelezwa. Naomba niwahakikishe tu kwamba Wizara imeyashughulikia na kwa sababu yalikuwa yanagusa maeneo mengi, ndiyo maana ilikwenda kuwa chini ya Wizara ya Waziri Mkuu.
Kwa hiyo, yale ambayo yanatugusa, yapo, tumeainisha na tutayatoa wakati wa hotuba ya bajeti ya kwetu. Kwa hiyo, niseme tu kwamba kila ambacho kimezungumziwa tuko tunaendelea nacho kukifanyia kazi tukijua wazi kabisa kwamba bila kufanya utatuzi huu itatuletea shida katika namna bora ya kupanga maendeleo katika Wizara na katika Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine ambalo limezungumziwa ni la kiusalama zaidi, kwenye usalama wa wavuvi ndani ya ziwa. Waziri mwenye dhamana tayari alishalichukua nalo linafanyiwa kazi kuhakikisha kwamba usalama wa wavuvi wetu unakuwa katika hali ambayo ni ya ulinzi zaidi. Bahati nzuri Waziri mwenye dhamana naye ana interest katika hilo. Naomba kusema tu kwamba tuko pamoja katika hilo.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAAZI: Niliambiwa dakika kumi, siyo tano Mheshimiwa.
NAIBU SPIKA: Ni kumi, ulishagongewa ya kwanza tayari.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia katika Bunge lako Tukufu, naomba nianze kwanza kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa fursa aliyonipa ya afya njema na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kusema yale nitakayoyasema ikiwa ni katika hali ya kujibu baadhi ya hoja za Wabunge ambazo wamezitoa na nyingi tutazijibu kwa maandishi na watapata nakala. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nichukue fursa hii pia kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo ameniamini na kunipa fursa ya kuweza kuniteua kuwa Naibu Waziri katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na niseme sitamuangusha. Kwa kupitia kwake pia niwashukuru sana wananchi wa Ilemela ambao wamenipa dhamana hii ya kuwawakilisha Bungeni na hatimaye Mheshimiwa Rais akanipa wadhifa mwingine wa kuweza kumsaidia katika Wizara niliyoitaja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuwa mwanamke wa kwanza kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais. Ni wazi atatuwakilisha vizuri na ameonyesha njia kwa namna alivyoanza. Nimpongeze pia Waziri Mkuu kwa kuteuliwa kwake na hasa wananchi wa Jimbo lake la Ruangwa kwa kumchagua kuwa Mbunge na hatimaye akateuliwa kuwa Waziri Mkuu na Bunge hili likamthibitisha. Niwapongeze Mawaziri na Naibu Mawaziri wote ambao wamechaguliwa. Nimpongeze Spika pamoja na Naibu Spika na Wabunge wote kwa nyadhifa zenu ambao mnategemewa sana na wananchi kwa sababu ya kuwapa ridhaa kwa hiyo wana matumaini makubwa kutoka kwenu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, shukurani zangu pia zimwendee sana Waziri na mtani wangu Mheshimiwa William Lukuvi kwa ushirikiano anaonipa katika kufanya kazi. Ni muda mfupi tu ambao tumekuwa pamoja naye lakini najisikia kuwa na faraja kubwa kwa sababu ni mentor mzuri ambaye anaweza kukuelekeza, akakushirikisha na ukaweza kufanya kazi vizuri. Na mimi nasema nitatoa ushirikiano kwake wakati wote kwa namna ambavyo anaelekeza nadhani imenifanya pia nitambue na nielewe Wizara kwa muda mfupi, nasema tutafanya kazi vizuri.
Pia niwashukuru watendaji wote wa Wizara pamoja na taasisi na mashirika yaliyoko chini ya Wizara wamekuwa na ushirikiano mzuri katika kufanya kazi hizi na hatimaye kwa muda mfupi sana huduma katika Wizara zimeboreka na watu wanahudumiwa vizuri na mrejesho tunaupata. Kwa hiyo, namshukuru sana Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Wakurugenzi na watendaji wote walioko katika idara nilizozitaja.
Aidha, pia nishukuru sana Ofisi ya TAMISEMI ambayo nayo tumekuwa tukishirikiana sana katika kutatua kero mbalimbali. Ardhi ni suala mtambuka na mambo mengi yanaletwa ardhi lakini yanagusa Wizara nyingi, kwa hiyo, nishukuru kwa hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika shukrani zangu nisisahau familia yangu, namshukuru sana mume wangu Julius Mabula, watoto wangu David, Javine, Diana na Dorothy, baba na mama wazazi Silvester Lubala ambao wameweza kunilea na kunifanya niwe kama nilivyo. Nashukuru ndugu, jamaa na marafiki ambao wote wamekuwa karibu sana katika kunitia moyo na kuweza kufanya kazi kwa umoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru Wabunge wote wa Mkoa wa Mwanza ambao tunashirikiana sana katika kazi zetu kuhakikisha kwamba Mkoa unakwenda vizuri. Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawashukuru viongozi wa dini madhehebu yote Mapadri, Mashehe, Maaskofu katika madhehebu mbalimbali ambao kwa muda wote wamekuwa wakiniombea na kunipa ushauri wa kimwili na kiroho na wamenifanya kwa kweli nisimame imara katika kazi zangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie shukurani zangu si kwa umuhimu kwa kukishukuru sana Chama changu ambacho kimeniamini kikaniteua na kunifanya nigombee katika Jimbo ambalo kwa miaka mitano tulikuwa tumepangisha lakini mpangaji akashindwa masharti ya upangaji tumemwambia apumzike ili tuweze kuendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani zangu naomba sasa nianze kujibu baadhi ya hoja ambazo zimetolewa na Wabunge katika michango yao ya maandishi na wengine kwa kuzungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuzungumzia ile taarifa ya Kambi ya Upinzani ambayo Waziri Kivuli aliiwasilisha hapa na nimshukuru tu kwamba taarifa yake ilikuwa ni nzuri kwa jinsi alivyoileta ina changamoto na mambo ambayo ameyasema hapa tutakwenda kuyatolea taarifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa ya Upinzani imezungumzia suala la uporaji holela wa ardhi katika maeneo mbalimbali, wamezungumzia ufisadi wa ardhi unaofanywa na viongozi na hakuna hatua zinazochukuliwa na wamezungumza kuhusu watu wa chache kuhodhi ardhi. Katika haya yote niseme utoaji wa ardhi kwa wawekezaji unazingatia zaidi sheria za nchi. Wizara inaelekeza mamlaka ya ugawaji kuzingatia sheria hiyo na Wizara imekuwa ikilisimamia hilo na imetoa mwongozo kwa Wakuu wote wa Wilaya ili kupitia katika vikao vyao ili ardhi isitolewe kiholela kama ambavyo imekuwa ikileta migogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia hatua zinachukuliwa kwa ardhi ambayo inapatikana kinyume na utaratibu. Wizara imeagiza Halmashauri zote nchini kufanya ukaguzi na uhakiki wa mashamba pamoja na viwanja ili kuweza kuratibu na kuona yapi ambayo yanamilikiwa isivyo kihalali ili hatua ziweze kuchukuliwa. Katika kutekeleza hilo pia ni wazi wote ni mashahidi tumeandaa kitabu ambacho kila mmoja anacho kimeainisha migogoro yote ambayo ipo. Mingine kweli inatokana na watu kukiuka taratibu, lakini mingine pia ni kwa utendaji pengine ambao umekiuka maadili ya kazi kwa watendaji wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la fidia ambalo amelizungumzia. Sheria ya Ardhi na kanuni zake zimeweka utaratibu wa kukadiria na kulipa fidia ya ardhi na fidia yake inatofautiana kutegemeana na eneo ambapo ardhi ipo. Kwa hiyo, kuna ardhi nyingine unakuta bei yake iko juu na nyingine iko chini. Pia hapa tutambue kuna wengine ambao wanalalamika lakini ardhi zao zilitwaliwa kabla ya ile sheria ya mwaka 2002 ambayo imeingiza ardhi pia kuweza kuthamanishwa. Kwa hiyo, wengi wanarudi kudai kuongezewa fidia lakini wakati huo huo walishathaminishwa kwa sheria ya kabla ya sheria mpya ambayo imeingiza na ardhi kuwemo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la ukaguzi wa ardhi ambalo limetolewa na Mheshimiwa Mdee, lakini na hapa mmeliongelea. Niseme Wizara ilishaanzisha kitengo kinachoshughulikia ardhi kwa ajili ya uwekezaji na pia imeziagiza Halmashauri zote nchini kufanya ukaguzi wa mashamba. Hii tunayofanya katika kunyang‟anya baadhi ya mashamba ambayo yametelekezwa sehemu kubwa pia tutachukua ili kuweza kuwa na akiba ya ardhi katika mtazamo huo kwa sababu siyo yote itakayogawiwa kwa wananchi na siyo yote ambayo watapewa tena wawekezaji lazima tutakuwa na sehemu ambayo itakuwa ni kwa ajili ya akiba kwa matumizi ya baadaye.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kutolipwa fidia ambalo limezungumziwa na hasa wamezungumzia pia maeneo ya jeshi, walizungumzia maeneo ya Kaboya na maeneo mengine yako Mwanza, Ilemela na mengine yametajwa eneo la Kusini. Niseme Waziri wa Ulinzi wakati anazungumzia aliainisha vizuri kabisa namna ambavyo wanakwenda kulipa fidia katika ile migogoro ambayo wanatofautiana sana kati ya jeshi na watu. Kwa hiyo, niseme jeshi limeweka utaratibu wa kutambua mipaka yao na kujipanga katika kulipa fidia. Wameliweka wazi hili na nisingependa kulirudia kwa sababu tayari iko kwenye hotuba ya Waziri wa Ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumziwa suala la wananchi wa Kata ya Kahororo kutolipwa fidia. Tukumbuke kwamba maeneo mengi ambayo yanachukuliwa na wawekezaji au taasisi mbalimbali suala la kulipa fidia linakuwa siyo suala la Wizara ya Ardhi ni la mwekezaji au taasisi inayochukua. Hili suala la Kahororo ni suala la Mamlaka ya Maji ya Bukoba ambapo thamani yake ni shilingi 1,961,609,000. Kwa hiyo, hizi zinatakiwa kulipwa kwa wale wananchi kwa kadri walivyothaminishwa katika uthamini uliofanyika mwaka 2014 kwa wananchi 186 na kiasi hiki kinatakiwa kulipwa.
Kwa hiyo, suala la ulipaji wa fidia lazima pia tuangalie ni nani anayehusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara ilishatoa Waraka kwamba hatutapokea jedwali lolote linalotaka watu waliofanyiwa uthamini kwa ajili ya kulipwa fidia kama hatutaridhishwa au kuhakikishiwa kwamba kuna pesa iliyotengwa. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Halmashauri zote wakileta madai yoyote ya fidia na wakitaka wathamini waende ni lazima tuwe tumejiridhisha kwamba kuna pesa imetengwa na watu watalipwa ili tuweze kufanya kazi hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna maeneo ya EPZ ambayo nayo yanadaiwa fidia. Kuna baadhi ambayo yalichukuliwa na yalikuwa yanalipwa fidia kulingana namna fedha zinavyopatikana. Maeneo ambayo yamecheleweshewa fidia kwa muda mrefu Serikali itaangalia uwezekano wa kuyarejesha mikononi mwa wananchi ili yaweze kutumika kwa kazi nyingine kwa sababu imekuwa ni kero kubwa na wananchi wamekuwa wakilalamika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu makampuni makubwa ya nje kuhodhi maeneo sehemu mbalimbali. Niseme tu Serikali inafanyia kazi orodha ya mashamba kama tulivyosema tayari tumeshaliweka katika utaratibu huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumzia pia suala la Mabaraza ya Ardhi na hili limezungumzwa na Wabunge wengi kwa uchungu sana. Naomba niseme tu kwamba ni wazi kama ilivyozungumziwa Mabaraza ya Ardhi hayako ya kutosha lakini hayana watendaji wa kutosha na kesi zake zinakaa kwa muda mrefu. Niseme tu kwa mwaka huu tumepeleka maombi maalum kwenye Wizara inayohusika kuomba tupatiwe Wenyeviti kwa ajili ya Mabaraza hayo yatakayofunguliwa. Tutafungua Mabaraza 47 na tutaanza na matano. Katika kuyafungua Mabaraza hayo kuna maeneo mengine ambayo yanahitaji ushirikiano wa Wilaya husika kwa sababu shughuli ya kuwa na maeneo na ofisi kila mahali inakuwa na ugumu wake kulingana na rasilimali zilizopo. Hata hivyo, tumebaini mahitaji halisi ya Mabaraza haya kwa lengo la kuboresha na tayari vifaa mbalimbali vimeanza kupelekwa katika maeneo kusudiwa. Aidha, kuhusu watumishi kama nilivyosema tumewakilisha ombi maalum.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme katika suala la Mabaraza ya Ardhi naomba tu tuwe na imani kwamba tunakwenda kulitatua tatizo hilo muda ambao si mrefu kuanzia sasa ili wananchi waweze kupata haki kwa wakati. Pia tutaangalia katika zile Wilaya kama watakuwa hawajapangiwa kuwekewa Baraza ambapo unakuta Wilaya moja inahudumia Wilaya zaidi ya tatu au nne, tutaangalia ni Wilaya gani ambayo ina kesi nyingi na inahitaji huduma hiyo kwa haraka. Kwa hiyo, tutaangalia badala ya Mwenyekiti kuwa katika eneo ambalo halina kesi nyingi basi itabidi tumhamishie katika eneo ambalo lina kesi nyingi ili aweze kuhudumia na atakuwa anakwenda kama visiting chairperson kwenye lile eneo kwa maana ya Mwenyekiti wa Baraza. Kwa hiyo, tuseme tu kwamba hili tutalifanyia kazi kulingana na namna ambavyo tutakuwa tumeyapata. Kwa hiyo, tunaanza na hayo ambayo tayari yapo matano, lakini yale mengine 47 yote yako katika mchakato mzuri wa kuweza kuyaanzisha, kote tutakwenda kuanzisha kama ambavyo tumesema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la National Housing. Kambi ya Upinzani kwenye hotuba yao nao wamelizungumza, lakini wachangiaji wengi sana pia wamezungumzia suala hili na wamezungumza kwa uchungu sana. Niseme walikuwa na haki ya kuyasema hayo yote kwa sababu National Housing ni kioo cha jamii na ni shirika pekee baada ya uhuru linafanya vizuri zaidi kuliko mengine yaliyoanzishwa kipindi hicho na mtakumbuka lilianzishwa mwaka 1962 baada tu ya uhuru. Kazi wanayoifanya sasa na wote ni mashahidi, mmeweza kusifia msimamizi wa shirika hilo lakini tuseme pongezi hizo zinaenda kwa watumishi wote katika idara husika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wamezungumza sana kwamba nyumba zinazosemwa ni za gharama nafuu si za gharama nafuu. Naweza kukubaliana na wanachozungumza kwa sababu ya hali halisi ya namna ambavyo National Housing wanavyopata maeneo yale na namna wanavyohangaika na miundombinu. Kama Wizara tumetoa maelekezo, tumesema kama National Housing sasa wanataka kujenga nyumba za gharama nafuu ni lazima waendelee kuwa wabunifu, waendelee kufanya utafiti kuweza kujua ni kwa namna gani watajenga nyumba za gharama nafuu kwa kuangalia vifaa. Achilia mbali lile suala la VAT ambalo tumelizungumzia, hili bado tunalizungumza Kiserikali kuweza kuona ni jinsi gani VAT itakuwa waved ili waweze kupata nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa sasa hivi tunaloangalia ni namna ya kushirikisha taasisi zingine kama TANESCO, Idara ya Maji, Idara ya Ujenzi (barabara) ambao ni Halmashauri zenyewe, waweze kufanya maandalizi ya ile miundombinu mapema ili National Housing wanapokwenda kule basi waweze kufanya kazi kwa pamoja. Lingine pia Halmashauri zetu pamoja na kwamba tunalalamikia National Housing kutowafikia, lakini bado hatujawapa fursa ya kuweza kuja kupata maeneo ambayo yatapunguza gharama. Kwa sababu wakija pale NHC wanatakiwa walipe fidia, watengeneze miundombinu hiyo, tumewaambia wajipange vizuri na wafanye networking na mashirika mengine ambayo yanashughulika na huduma nilizozisema ili waweze kuona ni jinsi gani hizo nyumba zitapungua gharama kulingana na namna ambavyo wamejipanga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa NHC wameshafikia Halmashauri 25 na wameshajenga nyumba ziipatazo 1,076 kwa maana ya zile za gharama nafuu. Kwa hiyo, niseme kwamba wapo katika utaratibu ambao unakwenda sambamba na mahitaji jinsi yalivyo ili kuweza kuona wanafikia wananchi kutegemeana na hitaji la Halmashauri. Niwaombe Halmashauri ambazo ziko tayari katika hilo basi waweze kuwapa nafasi ya kuweza kufika katika maeneo haya na kuwapa maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumzia hati za kimila kutotambulika. Naomba niwataarifu tu Waheshimiwa Wabunge kwamba hati za kimila kuna Benki ambazo tayari zinazitambua na zinapokea. Ttunayo benki ya CRDB, TIB, Exim Bank, NMB, Meru Community Bank ambazo tayari zimeshazitambua hizi hati za kimilila na zinatoa mikopo. Niseme haya yote yanafanyika na bado Serikali inaendelea kuongea na taasisi za fedha ili waweze kuthamini na kutambua kwamba zile hati ni hati ambazo zinahitaji kutambulika kama ambavyo benki zingine zimeanza kuzitambua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumzia masuala ya upangaji miji na huduma za jamii katika maeneo mbalimbali. Uvamizi wa maeneo bila kuwa na mipango mizuri ya matumizi bora ya ardhi hatutafika. Kama tulivyosema ni asilimia 15 tu ya ardhi ambayo imepangwa lakini ni jukumu pia la Halmashauri zetu kupima ardhi. Halmashuri zetu zinapaswa kutenga bajeti kidogo kidogo angalau wakapima kwenye maeneo yao. Tukikaa tukisubiri Wizara tutafanya kazi hiyo lakini itatuchukua muda mrefu.
Kwa hiyo, niombe Halmashauri zetu ziweze pia kuchukua wasaa wa kuweza kuyapima yale maeneo na kuweka matumizi bora ya ardhi ili kupunguza migogoro hii ambayo ipo. Kwa sababu kama tutaachia Wizara, kazi itafanyika kama tulivyoanza katika Wilaya ya Kilombero, Ulanga na Malinyi lakini tumeona kwamba huu ni mradi wa miaka mitatu ambayo ni mingi sana tutafikia vipi maeneo yote kama mlivyosema. Niseme hilo ni la kwetu sote tushirikiane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kutokuwa na Maafisa Ardhi Wateule, Halmashauri pendekezeni majina ya wale ambao wamefikia sifa hizo, mlete kwa Kamishina. Kwa sababu tayari tunao Makamishna Wasaidizi kwenye Kanda nane, watafanya kazi ya kuwateua watumishi hao ili waweze kufanya kazi hiyo.
Suala la upungufu wa watumishi bado tunalifanyia kazi kama nilivyosema pia tumeomba watumishi wengine waweze kuongezwa katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba mambo yaliyozungumzwa ni mengi ambayo yanahitaji pia kuwa na utulivu katika kuweza kuyapitia moja baada ya lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa ambalo nataka kusema ni kwamba masuala haya na hasa ya upimaji na mipango miji, tuna master plan ambazo zimeandaliwa katika miji yetu ya Mwanza, Arusha, Dar es Salaam ambao ulikuwa umeharibika sana unaandaliwa upya kwa kuzingatia mpango kabambe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana tuwaelimishe wananchi wetu wasiwekeze katika maeneo ambayo watakuja kupata shida baadaye kwa sababu master plan zinakuwa zimeandaliwa lazima waangalie waweze kujua katika eneo lake katika mpango uliopo panatakiwa kujengwa nini? Kwa hiyo, kama ni suala la umilikishaji na uendelezaji aweze kuendeleza katika hali halisi ambayo ndiyo mpango uliopangwa ili asijepata hasara baadaye anaambiwa abomolewe kwa sababu amejenga kinyume na taratibu au hakuzingatia mpango mji kwa kule ambako tayari mipango miji imeandaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge wa Misenyi amezungumzia habari ya kupanga mji mzuri kule kwao. Eneo lolote ambalo wamejiandaa katika kuweka kamji kadogo kazuri katakakofuata sheria na taratibu walete, Wizara ipo tayari tutasaidiana pia na wenzetu wa National Housing kuhakikisha kwamba huo mji unapangika vizuri na unajengwa majengo mazuri. Hata kama siyo National Housing tutaangalia pia nani anaweza akafanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Wabunge walilalamikia kuhusu ubovu wa majengo yanayojengwa na kulazimu kubomolewa. Naomba niwaambie, katika jengo lililobomolewa pale Dar es Salaam National Housing hakuwa amejenga yeye lilijengwa na mtu mwingine, majengo yote ya Nationa Housing yanakwenda vizuri. Kwa hiyo, wale wanaotaka kuwa na miji mizuri bado msisite kutumia Shirika la Taifa ambalo linaweza likafanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamejadiliwa lakini niseme haya ambayo nimeyadodosa tu kwa kuyapitia moja moja, kidogo kidogo bado niseme kwamba tutayajibu yote na Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa na yeye atajibu baadhi ya hoja. Niseme kwa wale wanaojenga maeneo yasiyofaa na kupatiwa huduma za maji, umeme na kadhalika, utoaji wa huduma kwa wakazi waliojenga maeneo hatarishi unafanywa na mamlaka na taasisi kwa kutoa huduma kwa msingi wa kibiashara na hata wale waliobomolewa ambao pengine walikuwa wana hati, Wizara ilishawaambia walete ili tuweze kutambua. Kama alikuwa na hati halali ya Wizara, tunajaribu kupitia na kuweza kuona tutawapa alternative ipi ya kuweza kuwapatia viwanja vingine. Habari ya kuwekewa maji, umeme isiwe ni sababu ya kujenga kwenye maeneo ambayo ni hatarishi. Wale wanafanya kazi zao kibiashara ukimwambia alete maji analeta kwa sababu anajua tu kwamba ni eneo ambalo anapeleka huduma. Kwa hiyo, niseme tupo pamoja katika kuhakikisha tunapanga miji yetu ili tuweze kuona kwamba ni jinsi gani tutakwenda pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala zima ambalo tumesema ni la utatuzi wa migogoro ambalo Waziri wangu atalizungumzia kwa kirefu. Hili suala ni mtambuka na kama ambavyo tumelieleza tutakwenda kukaa pamoja na Wizara zinazohusika ambazo ni Ofisi ya Rais (TAMISEMI), Maliasili na Utalii, Kilimo, Uvuvi na Mifugo na Maji tuweze kuona kwa sababu migogoro mingi imekuja kwenye Wizara lakini ukiangalia kitabu chetu tulikuwa tunaainisha pia kuona kwamba mgogoro huu utatatuliwa na Wizara ngapi, kama ni ya kwetu tumeonesha na Wizara nyingine anayofuatia tumeionesha. Haya yatafanyika katika utaratibu ambao utakuwa umewekwa vizuri ambao utatusaidia sisi sote kuepuka hiyo migogoro ambayo inajitokeza mara kwa mara na si lengo la Serikali kuweza kusema kwamba tuweze kuhatarisha maisha ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba haya yote tunayokwenda kuyafanya tunategemea zaidi ushirikiano wa Wabunge. Tayari kama Wizara tumeshawezesha kwa maana ya kupata zile nyaraka muhimu. Kwa hiyo, tunategemea pia mtakuwa ni sehemu ya utoaji wa elimu. Kwa sababu siku zote tunasema ardhi ni mtaji bila kufahamu sheria na kanuni zinazotawala ardhi bado itakuwa ni shida. Kwa hiyo, nyaraka hizo ni nyenzo mojawapo ambayo tumeitoa itakayotusaidia sisi sote, Wabunge pamoja na Waziri mwenye dhamana katika maeneo hayo ili kuweza kuona kwamba kazi hii tunaifanya katika muda muda mfupi kwa kusaidiana na hatuzalishi migogoro mingine kwa sababu taratibu tutakuwa tumezizingatia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nimalizie kwa kuwashukuru sana Wabunge kwa ushirikiano wao na Wizara. Baada ya kuwa tumepokea hoja na migogoro, Wizara itaishughulikia yote na baadaye tutaona namna bora ya kuweza kuona kwamba Taifa ambalo halina mgogoro linapatikana. Kwa sababu kazi tuliyopewa na Mheshimiwa Rais ni kuhakikisha migogoro iliyopo inakwisha na tusizalishe mingine lakini ni mimi na wewe ambao tutakwenda kuhakikisha migogoro inakwisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nimuachie Mheshimiwa Waziri aweze kuendelea kwa sababu najua kila ambalo limeandikwa litafanyiwa kazi na litakwenda kutolewa ufafanuzi kama ambavyo tumepanga. Nashukuru kwa kunisikiliza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa fursa hii ambayo amenipa na kunipa afya njema na hatimaye kuweza kusimama katika Bunge lako Tukufu na kuweza kujibu baadhi ya hoja ambazo zimetolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea, naomba nichukue fursa hii kutoa pole kwa wananchi wa Mkoa wa Mwanza na mikoa ya jirani ambao jana wamepatwa na tetemeko na hususan Jimbo langu ambalo karibu Kata saba zote zimepitiwa na tetemeko hilo. Tunamshukuru Mungu kwamba madhara hayakuwa makubwa sana na tunamwomba Mungu amrehemu yule Askari ambaye amepoteza maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Spika, Naibu Spika, pamoja na Wenyeviti wote wa Bunge hili kwa kazi nzuri ambayo mnaifanya na mmekuwa mkituongoza vizuri katika shughuli nzima ya kuendesha Bunge letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nampongeza sana Mwenyekiti wa Kamati yetu pamoja na Makamu wake ambao wamekuwa wakitupa ushauri kupitia Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Ardhi, Maliasili na Utalii ambayo tumekuwa tukifanyanao kazi vizuri. Namshukuru sana pia Waziri Kivuli ambaye naye amefanya kazi nzuri katika kuwasilisha hotuba yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nachukua fursa hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo langu la Ilemela kwa kuniamini. Nashukuru Chama cha Mapinduzi kwa kuniamini, lakini Serikali pamoja na Viongozi wa Dini ambao wamekuwa pamoja nasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naungana na wachangiaji wote waliotangulia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri sana ambayo anaifanya. Kwa kweli, amekuwa ni kiongozi wa mfano, kiongozi wa vitendo, kiongozi ambaye anasimamia kauli zake. Nasi wasaidizi wake tunasema tutakuwa tayari kumsaidia pale ambapo tunahitaji kusaidia kwa kadiri alivyotuamini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri wetu Mkuu pamoja na Makamu wa Rais. Kwa kweli wamekuwa wakitupa ushirikiano mzuri na kutupa maelekezo mazuri ya kuweza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapokea pongezi zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Naomba nichukue fursa hii kuwashukuru sana, lakini niseme pongezi hizo hazikutustahili sisi peke yetu, ni sisi pamoja na ninyi Waheshimiwa Wabunge kwa sababu, ushirikiano mliotupa umefanya pia kazi yetu iwe rahisi. Kwa hiyo, nasi tunawashukuru sana. Maandiko yanasema, “moyo usio na shukrani hukausha mema yote.” Hivyo hatuna budi kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa ushirikiano wenu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani na pongezi mlizozitoa, kwetu sisi ndani ya Wizara ni chachu ya kuzidi kuongeza kasi ya kutenda kazi vizuri na kuweza kusaidia jamii ambayo muda wote inategemea utendaji wetu. Nawashukuru sana pia Watendaji wetu ndani ya Wizara ambao wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana katika kuona kwamba, shughuli hizi zinafanyika vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee kabisa, nimshukuru sana Waziri wangu, Mheshimiwa Lukuvi. Ni Waziri ambaye amekuwa ni mentor wangu mzuri, ni kiongozi ambaye anaweza kuelekeza vizuri, ni kiongozi ambaye anasimamia maamuzi, ni kiongozi ambaye kama ni mwanafunzi mzuri, kwa kweli utafuata nyayo. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana kwa sababu umenifanya niwe kama nilivyo katika Wizara hii ambayo ina changamoto nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa niseme kwamba Sekta ya Ardhi inakabiliwa na changamoto nyingi. Wote ni mashuhuda, tumeona namna ambavyo Waheshimiwa mmechangia katika kutoa hoja zenu. Katika michango yenu jumla ya Waheshimiwa Wabunge 77 wamechangia; 40 wamechangia kwa njia ya kuzungumza na 37 wametoa kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu kubwa ya michango ya Waheshimiwa Wabunge waliyoitoa, imejikita katika suala zima la utawala wa ardhi ambapo sehemu hii inahusu migogoro ya matumizi ya ardhi baina ya watumiaji mbalimbali wakiwemo wakulima, wafugaji, wawekezaji na hifadhi zetu ambazo zipo nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kuna suala la kutolipwa kwa fidia kwa wakati kama ambavyo mmesema, lakini kuna ucheleweshwaji wa utoaji wa Hakimiliki za Ardhi. Yote haya yako katika utawala wa ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ambayo pia imezungumziwa na Waheshimiwa Wabunge wengi sana ni suala zima la upimaji na ramani. Katika maeneo haya limezungumziwa suala la uhaba wa wataalam wa upimaji na vitendea kazi, gharama kubwa za upimaji, umuhimu wa kuimarisha mipaka ya nchi, migogoro ya mipaka ya Vijiji, ya Kata, Wilaya kwa Wilaya, lakini pia migogoro kati ya wananchi kwenye vijiji pamoja na hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Mipango Miji, nako Waheshimiwa wengi wamezungumzia. Maeneo mengi waliyozungumzia upande huu walikuwa wakitoa kama ushauri; suala la kuharakisha zoezi la urasimishaji wa makazi katika miji mbalimbali ambalo tayari limekwishaanza; Waheshimiwa Wabunge wameishauri Wizara kuongeza kasi ya uaandaaji wa mipango kabambe, ushauri tumeupokea, lakini pia limezungumziwa suala la uhaba wa watumishi na vitendea kazi katika Halmashauri mbalimbali. Tunakiri uhaba huo upo na ni kikwazo kikubwa katika kupanga miji yetu ili kuwa na miji salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine lililozungumziwa na Waheshimiwa Wabunge, ni la maendeleo ya nyumba. Hili limezungumziwa na Waheshimiwa Wabunge wengi sana. Kubwa hapa lilizungumziwa kuhusu gharama kubwa za ujenzi wa nyumba kwa wananchi, imekuwa gharama ni kubwa kwa hiyo, vipato vyao ni vidogo na hawawezi kumudu kulingana na bei ambayo imewekwa na National Housing. Pia, mmezungumzia uhaba wa nyumba kwa watumishi katika maeneo hasa ya vijiji. Haya yote tumeyapokea kwa sababu ni michango; ni hali halisi ambayo ipo, lakini bado tutazungumzia majibu yake kwa baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo limezungumziwa ni suala la Mabaraza ya Ardhi na Nyumba katika Wilaya zetu. Upande huu umezungumziwa uhaba wa watumishi wa mabaraza katika Mabaraza yetu kwenye Wilaya, lakini pia mkazungumzia suala zima la azma ya Serikali ya kuwa na mabaraza haya katika kila wilaya. Ni kweli, hatujaweza kutimiza azma hiyo, lakini nia ya Serikali ni njema na tutaendelea kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa utangulizi wa maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyachangia, naomba sasa nianze kujibu hoja mbalimbali ambazo zimetolewa, nikianza na hoja kutoka kwenye Kamati yetu ya Bunge ya Kudumu ya Wizara ya Ardhi, Maliasili na Utalii ambayo imetoa hoja mbalimbali. La kwanza amezungumzia ufinyu wa bajeti katika Tume yetu ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi ambayo imekuwa ikipatiwa rasilimali kidogo kulingana na kazi wanazozifanya na ndivyo jinsi ambavyo mmeliona suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niwahakikishie kwamba Serikali imekuwa inatoa fedha kulingana na bajeti inavyopata katika Tume ile. Kwa sasa Tume ile inalo Fungu lake, inayo Vote yake Na. 3 ambayo sasa imeanza kutengewa bajeti kuanzia mwaka 2016. Mwanzoni ilikuwa iko ndani ya bajeti ya Wizara kwenye Fungu Na. 48, lakini kwa kasi ambayo yao na kazi wanayofanya, wameweza kufanya majukumu yao kulingana na pesa waliyopata na wanafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa mafungu kadiri yatakavyozidi kuongezeka, tutawaongezea kwa sababu Tume hii ni muhimu sana katika kufanya shughuli za upangaji miji yetu katika maeneo yetu hasa katika mipango ya matumizi bora ya ardhi. Kwa hiyo, niseme tu kwamba tumepokea maoni hayo na tutazidi kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha huu wa 2017/2018 Serikali imeipatia Tume vibali vya ajira kwa watu saba. Kwa sababu wakati mwingine pia utekelezaji wake haukuwa mzuri sana kwa sababu hawakuwa na personnel ya kutosha. Kwa hiyo, wataongeza wataalam wengine saba ambao ni kutoka katika kada mbalimbali kwenye eneo lao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali kupitia Wizara yangu itaendelea kuipatia Tume ushirikiano mzuri, hasa wa rasilimali fedha na watumishi pamoja na vitendea kazi ili waweze kufanya ile kazi ambayo wote tumeitambua kwamba ni muhimu, Tume hii ifanye kazi yake vizuri katika kusaidia katika mpango wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala pia la kuongeza kasi ya elimu kwa umma kwa matumizi ya ardhi ambayo yameonekana kwamba kwa watumiaji mbalimbali imekuwa ni shida. Katika kutekeleza jambo hili, majukumu ya kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi, ngazi ya Kata na Vijiji, Tume hutoa elimu kwa timu za usimamizi wa ardhi kwenye vijiji na hususan katika Halmashauri. Hili limekuwa likifanyika na kumekuwa na ushirikiano mzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, timu ya kusimamia mipango ya matumizi bora ya ardhi katika Wilaya hujengewa uwezo wa kuratibu na kupanga utekelezaji na usimamizi huu wa mipango ya matumizi bora ya ardhi nchini. Hivyo, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Tume ilitoa elimu katika Halmashauri 24 nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Tume imekuwa ikifanya kazi yake vizuri, pamoja na ufinyu wa bajeti ambao umekuwa ukitokea. Pia Tume hii huandaa vipindi maalum vya elimu kwa umma. Hii yote ni katika kupanua uelewa katika maeneo yetu ili kusaidia kujenga uelewa wa pamoja. Imekuwa ikitumia njia mbalimbali ikiwemo kutumia vyombo vya habari, maonesho ya Saba Saba, Nane Nane, Wiki ya Utumishi na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote yanafanyika ili kuweza kupanua wigo wa kutoa elimu. Vipindi hivi pia vimekuwa vikihusisha sheria, taratibu na miongozo ya kupanga na kusimamia matumizi bora ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango wa Elimu kwa Umma umeandaliwa kwa kushirikisha wadau wa matumizi ya ardhi kama Taasisi za Umma na Asasi Zisizo za Kiserikali. Care International Tanzania, Haki Elimu, Ardhi Oxfarm na Ujamaa Community Resource Team. Hawa wote wamekuwa wakishiriki katika zoezi hilo. Kwa hiyo, kazi inayofanyika ni nzuri kiasi kwamba ni kiasi cha kufuatilia tu zile programu zinapokuwepo ili watu waweze kujengewa uelewa mzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine wamezungumzia kuwa Serikali itenge fedha za kutosha ili kuyafikia maeneo mengi zaidi nchini yenye migogoro ya mipaka ya ardhi. Katika suala hili Serikali itaendelea kutenga fedha kadri zinavyopatikana. Aidha, Wizara pia itaendelea kushirikiana na wadau wa Sekta binafsi ili kufikia maeneo mengi katika kutoa elimu na masuala ya ardhi ili kuepusha migogoro hii. Kwa hiyo, Serikali peke yake haiwezi, ndiyo maana tunashirikisha sekta binafsi ambazo zipo katika taaluma hii ili kuweza kufikia wananchi wengi kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukosefu wa fedha pengine unakuwa nao ni kikwazo sana, lakini Serikali itaendelea kuishughulikia changamoto hii katika kuweza kupata rasilimali hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imetoa ushauri katika mambo mengi na sisi tunayachukua na tumeyapokea kama yalivyo, wamezungumzia suala la Serikali ihamasishe Halmashauri kukopa ili kutekeleza miradi ya kupima viwanja. Hilo tumelipokea. Kuwezesha Bodi ya Mfuko wa Fidia ya Ardhi iweze kutekeleza majukumu yake tumelipokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuhusu Wizara kuendelea kufanya kazi kwa pamoja na wadau wengine, tumelipokea na tunaendelea kulifanyia kazi; kuhusu Sheria ya Ardhi kwamba iboreshwe na kusimamiwa kikamilifu ili kuondoa migogoro baina ya watumiaji ardhi, huo ushauri tumeupokea, tunaendelea kuufanyia kazi; kuongeza kasi ya kutoa elimu nimesema tunaendelea, kwa hiyo, ushauri huo tumeupokea na tunaufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba Serikali itenge fedha za kutosha kwa ajili ya kuanzisha Mabaraza ya Ardhi. Kama nilivyosema kwenye utangulizi, nia ya Serikali ni kuwa na mabaraza haya katika nchi nzima. Tuseme tu kwamba kwa mujibu wa Sheria ya Mabaraza ya Ardhi ya Na.2 ya mwaka 2002, kila Wilaya inatakiwa kuwa na Baraza. Lengo la Serikali ni kuwa na Mabaraza haya katika kila Wilaya. Hadi kufikia 15 Mei, 2017 Serikali tayari ilikuwa imeshaunda Mabaraza 97 kati ya yale Mabaraza 100 tuliyokuwa tumekusudia kuweka, ambapo kati ya hayo Mabaraza 53 tayari yanatoa huduma; na Mabaraza 44 hayajaanza. Kwa hiyo, nia ya Serikali ni njema na tunaendelea kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali inatarajia kuajiri watumishi 291 na kati ya hao, watumishi 98 ni ajira mpya katika Mabaraza. Kwa hiyo, tuna imani tukishawapata hao, basi yale maeneo yote ambayo yana upungufu wa watumishi hao katika Sekta hiyo, watakuwa wamepata. Kwa hiyo, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge tuwe na uvumilivu, Serikali ina nia njema na itaweza kufanya haya yote kadri ya muda unavyoruhusu na bajeti inavyoruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilitolewa kwamba, Serikali iangalie namna ya kupunguza gharama za ujenzi wa nyumba za National Housing. Hili zimezungumzwa na wachangiaji wengi, lakini Kamati pia imelizungumza. Naomba niseme kwamba Serikali imepokea ushauri huu, lakini pamoja na hayo Mheshimiwa Rais alishatolea maelekezo, kwa sababu wengi walilalamikia gharama kwamba zimekuwa kubwa. Tumekuwa tukilieleza siku zote kwamba pengine gharama kubwa inachangiwa na National Housing kufanya kila kitu wao wenyewe; kwa kuweka miundombinu ya barabara, maji na umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, hili tayari Mheshimiwa Rais ameshalitolea maelekezo kwamba Taasisi zinazohusika na huduma, kabla National Housing hawajaweza kufanya uwekezaji wao, basi kama ni barabara iwe imeenda, miundombinu ya umeme iwe imesogea na maji yawe yamekwenda. Wakiweza kusongeza huduma hizo, ni wazi gharama ya nyumba itapungua. Kwa hiyo, hili linafanyiwa kazi na Mheshimiwa Rais ameshalichukulia hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili limefanyika hata kwenye hizi nyumba za Iyumbu zinazojengwa sasa hivi hapa, tayari maelekezo yalishatolewa. Kwa hiyo, nina imani kwamba kwa sababu maelekezo yamekwenda katika Halmashauri zote katika kutekeleza agizo la Mheshimiwa Rais, Waheshimiwa Wabunge ambao mnataka kuwekeza katika maeneo yenu kwa kuwashirikisha National Housing, basi nadhani tukitekeleza hayo pia kwao itakuwa ni rahisi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, National Housing wako tayari kwenda maeneo yote na siyo National Housing peke yake, hata Watumishi Housing ambao wanajenga nyumba za watumishi nao wanahitaji kuwa na miundombinu hiyo hiyo ambayo inatakiwa kuwekezwa. Hii itapunguza sana gharama za nyumba ambazo tunazungumzia. Kwa hiyo, hili tumelichukua na Rais amelitolea agizo na litatekelezwa kadri ambavyo miradi itakavyozidi kuwekezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilitaka Wizara ihakikishe Manispaa ya Dodoma inatekeleza dhima iliyokuwa ikifanywa na CDA na kupeleka huduma ya jamii ya miundombinu. Hii ilikuwa ni hoja ya Kamati na walizungumzia Iyumbu na nimeshaizungumzia. Kwa hiyo, suala la miundombinu limewekwa sawa.

Mheshimiwa Mwenyeiti, kuna suala lingine ambalo limezungumziwa, kuhusu kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Mipango Miji kwani kuna changamoto nyingi. Niseme tu kwamba Sheria Na. 8 ya 2007 inazipa Halmashauri zetu za Wilaya na Miji pamoja na Manispaa mamlaka ya kupanga na kudhibiti uendelezaji wa miji. Wizara kama msimamizi mkuu, kwa Waraka wake Na.1 wa mwaka 2006 unaoelekeza taratibu za kufuata katika kubadili matumizi ya ardhi na mgawanyo wa viwanja na mashamba, hili linasimamiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Wizara ilitoa Waraka Na. 4 mwaka 2006 ambao unatoa maelekezo ya miongozo ya udhibiti ya undelezaji miji. Kwa hiyo, jukumu hili bado liko katika Halmashauri zetu kwa sababu sheria zipo. Tukiangalia tu Wizara peke yake tunaweza pengine tukachelewa kudhibiti hili suala.

Mheshimiwa Mwenyeiti, naomba sana katika hili Halmashauri zetu Sheria Na. 8 ya mwaka 2007 hii ya Mipango Miji lazima isimamiwe katika maeneo hayo. Haya yote yataepusha hizo changamoto ambazo tunazisema. Kwa hiyo, Wizara kama msimamizi, tuko karibu sana na Halmashauri kushirikiana nazo, lakini Waheshimiwa Wabunge ni jukumu letu pia kuhakikisha kwamba tunapoona hali inakuwa siyo nzuri, kwa sababu tunahitaji miji iliyopangika na miji ambayo ni salama, ni jukumu letu pia kuwakumbusha wataalam wetu kuweza kusimamia mambo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la mipango kabambe ya miji ambayo inatakiwa isiishie kupanga tu miji mikubwa, bali ipanue wigo wake. Hili linafanyika na sasa hivi kuna kujumla ya mipango kabambe 26 ambayo iko katika hatua mbalimbali. Mpaka sasa mji wa Mtwara pamoja na Musoma mipango yake kabambe imekamilika toka mwezi Mei na Mheshimiwa Waziri alikwenda kuzindua. Kwa hiyo, mipango mingine bado iko kwenye mchakato na tutaendelea kufanya hivyo. Wizara imeandaa programu ya utayarishaji wa mipango kabambe kwa nchi mzima ikiwemo miji midogo ambayo inakua kwa kasi. Kwa hiyo, hili tunalichukulia kwa uzito wake na tutaendelea kulisimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa hoja za hotuba ya Waziri Kivuli, ametoa hoja nyingi sana. Niseme tu kwa ujumla wake pamoja na zile ambazo nimemaliza kuzijibu kwamba tunaandaa pia kitabu ambacho kitajibu hoja zote, maana kwa muda uliopo siwezi kuzijibu zote, nitajibu chache tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kupima ardhi ya Mkoa wa Morogoro kama mpango wa dharura ili kupunguza migogoro; wameongelea kwenye hotuba hiyo. Niseme tu Tume inaendelea na mipango ya matumizi bora ya ardhi. Kama nilivyosema awali na hata katika kujibu maswali tunapojibu, Morogoro ilichukuliwa kama eneo ambalo Serikali ilikuwa inaliangalia kwa jicho pana zaidi kutokana na migogoro yake iliyokuwepo. Ndiyo maana zile Wilaya tatu ambazo sasa tunapima ardhi yote, imeanzia Morogoro, ni kwa sababu ya tatizo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili nalo tunalichukua, hivyo vipande vya ardhi vyote vitapimwa na kuwekewa alama za kudumu ili kuweza kuepusha hii migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ambalo limeongelewa kwenye maeneo ya Hembeti, Ndimboho, Buguma, Mkindo, Kigugo, Kambara vilivyopo katika bonde la Mto Mgongola Wilaya ya Mvomero, nadhani Serikali itachukua taratibu zake vizuri kuweza kuona kwamba tunafanyaje, kwa sababu hali halisi kila mmoja anaifahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume inashirikiana na programu ya kurasimisha ardhi katika Wilaya tatu nilizowaambia. Kwa hiyo, hatua zinachukuliwa na tunaendelea. Vile vile Tume inashirikiana na Halmashauri za Wilaya Mvomero na asasi za kiraia kama ile ya PELUM Tanzania TFCG na IWASHI katika kutoa elimu. Lazima elimu iwafikie ili waweze kutambua ni nini kinatakiwa kufanyika. Kwa hiyo, haya yanafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, Kambi Rasmi imeongelea kuhusu changamoto kubwa ya kibajeti katika Wizara na wakashauri pengine Serikali iongeze nguvu katika kushirikiana na Sekta binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Urasimishaji katika eneo la Kimara ni mojawapo ya mfano ambao tunaweza kuusemea. Mradi huu lengo lake pia ulikuwa umekusudia kurasimisha viwanja 6,000, lakini mpaka tunavyoongelea sasa, viwanja 4,333 tayari vilikuwa vimeshapimwa na Hatimiliki zimetolewa 82 na kuna barabara ya urefu ya kilomita tisa imetengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile speed ndogo ya kutoa hati inachangiwa na wananchi wenyewe. Kama Wizara imeweza kupima viwanja 4,333 kati ya 6,000, ilikuwa imekusudiwa watu wote 4,333 wawe wamechukua hati. Sasa hiyo huwezi kusema kwamba ni tatizo la Wizara. Ni tatizo la wananchi ambalo tunasema tunawapa elimu ili waweze kuona manufaa ya kurasimishiwa maeneo yao ili pia waweze kutumia zile hati katika shughuli za maendeleo. Viwanja vimepimwa lakini watu hawachangii. Ni jukumu letu Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuhamasisha wananchi wetu kuchukua hati zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kwa wale wote ambao zoezi hili linaendelea ikiwemo na Mkoa wa Mwanza katika zile Wilaya za Nyamagana na Ilemela, lakini tunao wenzetu wa Musoma, Lindi, Kigoma, Ujiji na Sumbawanga; nawaomba sana, zoezi hili ni kwa nia njema ya kutaka kuwasaidia wananchi. Kwa hiyo, pale ambapo urasimishaji unafanyika, nawaomba sana wananchi, kwanza mchango siyo mkubwa ukilinganisha na gharama halisi ya upimaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba nia ya Serikali ni nzuri. Kwa hiyo, watumie fursa hii ya sasa ambayo ipo. Mkishaweka mipango kabambe katika maeneo yenu, unaweza kukuta urasimishaji tena hauna nafasi na tusingependa tufikie hapo. Kwa hiyo, hatua tuliyonayo sasa ni vizuri wananchi wanakaifanyia kazi iliwaweze kufaidika na zoezi hili linaloendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameongelea suala la migogoro kati ya mpaka wa Kisopa King’azi na Mloganzila; fidia ilishalipwa kama ambavyo ilikuwa imetajwa katika masuala mazima ya uendelezaji na hii iko katika Wilaya ya Kisarawe ambayo ilikuwa imeanzishwa kwa GN hiyo 117 ya tarehe 28 Novemba, 1980. Katika ule mgogoro uliokuwepo pale, wale ambao walikuwa wameendeleza walikuwa tayari Serikali imelifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa GN 69 ya 29/1/2016, eneo hilo la Ubungo ilimega sehemu ya Kinondoni ambayo ilijumuisha maeneo ya Kisopa na King’azi, Mloganzila hiyo ilikuwa ni chanzo cha migogoro. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa Wizara itashirikiana na TAMISEMI ili kupata suluhu ya mgogoro huu. Kwa sababu kama kunakuwa na mgongano wa GN au kunakuwa na mgongano wa kijiji na kijiji, bila kuwa na elimu kwa wale hasa walioko katika maeneo yale inaweza ikaleta shida; suala la mipaka wakati mwingine linakuwa lina shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi Wilaya mpya inapoanzishwa siku zote inakuwa na changamoto zake, hasa upande mmoja unaposhindwa kuridhia ama kuachia baadhi ya maeneo. Kwa hiyo, migogoro kama hii inakuwepo tu, lakini Serikali itaendelea kushirikiana na TAMISEMI kuhakikisha mgogoro huu unakwisha katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja nyingine inayosema Serikali imalize ufafanuzi kuhusu mgogoro wa mpaka kati ya vijiji na hifadhi ya wanyama Serengeti, ambayo imezungumziwa hasa katika maeneo ya Vijiji vya Marenga, Nyamakendo, Mbalimbali na vijiji vingine kama vilivyo, hivi vyote katika Wilaya ya Serengeti vina mgogoro na hifadhi kama ambavyo ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri tu Mheshimiwa Mbunge kuwa ni vema tukasubiri maamuzi ya Mahakama, sababu hili suala liko Mahakamani na hatuwezi kulitolea maamuzi hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine ambalo lilikuwa limezungumziwa na Kambi Rasmi ya Upinzani kwamba Serikali ieleze Bunge sababu za kuipa TRA mamlaka ya kukusanya kodi ya majengo ambayo ilikuwa ni chanzo muhimu kwa Halmashauri zetu. Tumesema TRA ilipewa jukumu la kukusanya kodi ya majengo ili kuimarisha mfumo wa ukusanyaji kodi. Hii yote ilipangwa kwa nia njema katika kurahisisha ukusanyaji maduhuli ya Serikali na zoezi limeanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile limezungumziwa suala zima la kupanga rates ambazo pengine wakati mwingine zinaweza kuwa ziko juu au zipangwe kulingana na viwango. Hii tumechukua kama ushauri ambao tunaweza kwenda kuufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumzia suala la kutatua migogoro ya eneo la mnada wa Pugu Kajiungeni na UKIVIUTA, Kipawa. Eneo la Mnada wa Pugu Kajiungeni lipo chini ya Wizara ya Kilimo na Mifugo na eneo hili limevamiwa na wananchi na kuendelezwa. Utatuzi wa mgogoro huu utahusisha wadau mbalimbali ikiwemo Wizara yenyewe ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba wavute subira kwa sababu itafanyiwa kazi. Vile vile kuhusu UVIKIUTA, suala hili lilifikishwa Mahakamani na Mahakama ilitoa ushindi kwa UKIVIUTA. Kwa hiyo, nalo tayari lilishatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna lingine limeongelewa kwamba Wizara iandae takwimu za hati ambazo zipo. Ushauri umezingatiwa, tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameongelea pia suala la Wakuu wa Wilaya kuingilia majukumu ya Mabaraza ya Ardhi. Suala hili, kwa mujibu wa Sheria ya Mabaraza ya Ardhi, Sura Na. 216 kama ambavyo imerejewa mwaka 2002, Mabaraza ya Ardhi na Nyumba Wilaya ni chombo huru cha kuamua migogoro ya ardhi. Hivyo haipaswi kuingiliwa na chombo chochote katika kutekeleza majukumu yake. Kwa hiyo, masuala haya yako kisheria na tunasema yataendelea kusimamiwa chini ya sheria husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kuhamisha ajira ya Watumishi wa Sekta ya Ardhi kutoka Halmashauri kwenda Serikali Kuu. Serikali itaendelea kutekeleza ile dhana ya D by D, hatuwezi kusema leo tunaibadilisha hapa kwa sababu tayari utekelezaji wake unakwenda vizuri na wote tunaona, lakini hayo yote yatafanyika kwa utaratibu ambao Serikali imepanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa kuhamisha ajira za watumishi katika Sekta ya Ardhi kutoka Halmashauri, unakinzana na dhana hii ambayo Wabunge wanaipendekeza. Ili kuongeza huduma kwa wananchi, Wizara imefungua ofisi za Kanda, kwa hiyo, tutashirikiana na Watumishi wa Ardhi kwenye Halmashauri kuona kwamba kazi hizi zinafanyika katika utaratibu mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia suala la Serikali kuwa na vipaumbele vya kutekeleza kulingana na mapato yake kuliko kuwa na vipaumbele vingi ambavyo wakati mwingine havitekelezeki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba Serikali imekuwa ikitekeleza majukumu yake kwa kuweka vipaumbele muhimu ikiwa ni pamoja na kutekeleza bajeti kulingana maoteo yanayopangwa katika projections zetu tunazozifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, suala la kuwa na vipaumbele vingi sidhani kama ni sahihi sana kwa sababu wakati mwingine unapanga ukitarajia kwamba maoteo yanakwenda kufanya kazi katika utaratibu uliopangwa. Isipokuwa wakati mwingine ufinyu wa bajeti unafanya usitekeleze jukumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kusema kwamba usipange, maana hizi ni projection ambazo ni lazima uziandae. Kwa hiyo, unapoandaa unategemea pia utapata pesa na tunafanya kazi kwa cash budget, kwa hiyo, lazima pia haya nayo tuyazingatie. Pia fedha ya Serikali inatolewa kutegemeana na makusanyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nawaomba tu Waheshimiwa Wabunge, tusisitize katika kukusanya pato la Serikali ili tuweze kuhudumia bajeti zetu ambazo tumezipitisha. Ni vema wananchi walipe kodi zao kwa wakati ili kuwezesha Serikali kutekeleza majukumu yake. Usipolipa kodi kwa wakati, matokeo yake shida inakuwa ni hiyo. Sasa hivi watu mpaka wafuatwe na Polisi, Summons za Mahakama ndiyo walipe kodi. Kwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tukiwa wazalendo kweli, kila mmoja akatimiza wajibu wake; unajua unatakiwa kulipa kodi ya ardhi kila mwaka, wewe lipa. Kwa nini unangoja mpaka uletewe Summons? Wakipelekewa Summons za Mahakamani, kesho yake unaona foleni kubwa iko kwenye Ofisi za Wizara. Sasa hivi ukienda TRA hapaingiliki katika zile kodi za majengo. Watu wamejaa pale, wanashinda pale. Kwa nini unangoja mpaka ufikie hatua hiyo? Lipa kodi kwa wakati ili uondoe usumbufu. Tukiweza kuwajibika, haya yote hayatakuwa tena na usumbufu katika utekelezaji. Kwa hiyo, ni jukumu letu kuona ni jinsi gani tunasaidiana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupitia hoja mbalimbali za Kambi Rasmi ya Upinzani, naomba sasa nianze kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge mmoja mmoja na nitaziunganisha zile zinazofanana ili kwenda na wakati na kwa zile ambazo nitakuwa nimezijibu wakati najibu hoja za Kamati pamoja na Kambi Rasmi ya Upinzani, nitaziruka na sitazirudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Mheshimiwa Abdallah Ulega na Mheshimiwa Zuberi Kuchauka, walikuwa wanazungumzia suala la kupunguza urasimu katika upimaji ardhi kwa wananchi wa vijiji ili kuwaondolea usumbufu. Wizara yangu imepunguza sana gharama. Walikuwa wanazungumzia gharama na kupunguza urasimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu imepunguza sana gharama na hata kama kwenye bajeti mmesikia, tumezidi kupunguza gharama. Lengo letu ni kuhakikisha usumbufu kwa wananchi haupo. Kwa hiyo, ni jukumu letu kuwahamasisha wananchi wetu waweze kuona umuhimu wa kupima maeneo yao ili waweze kuwa na umiliki halali ambao utawasaidia pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Wizara ni kuendelea kuhakikisha tunawawezesha wananchi. Unamwezesha kwa kutumia ile ardhi yake; ukiweza kumpa Hakimiliki kisheria tayari utakuwa umemsaidia. Kwa hiyo, niseme kwamba Wizara itaendelea na utaratibu wa kupata vifaa vya upimaji ili waweze kupimiwa kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa habari njema tu, kama mmesoma magazeti ya jana, tayari kuna tender imetangazwa kwa ajili ya ununuzi wa vifaa hivyo na ile No objection tuliyokuwa tunaisubiria kutoka World Bank, nayo tayari imetoka. Kwa hiyo, tuna uhakika vifaa hivi mtakwenda
kuvipata na kazi itafanyika na watu watapimiwa, tuwahamasishe tu wajitokeze kwa wingi ili waweze kupimiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine ambalo limeongelewa na Wabunge kama wanane; ameongea Mheshimiwa Mama Makilagi, Mheshimiwa Paresso, Mheshimiwa Shekilindi, Mheshimiwa Mwassa, Mheshimiwa Bashungwa, Mheshimiwa Bilakatwe, Mheshimiwa Chumi na Mheshimiwa Allan. Wamezungumzia kwamba Serikali itenge fedha kwa ajili ya kuanzisha mabaraza. Nilishalizungumzia lakini bado limejirudia. Lengo letu bado lipo pale pale, tumechukua hoja zetu na tutafanya kama ambavyo imekusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ule utaratibu wa maeneo ambayo pengine hayana Wenyeviti, nachukua fursa hii kumwomba sana Mkuu wa Mkoa wa Singida pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Tabora; tunajua huko kuna matatizo na Wenyeviti ambao muda wao tayari ni kama ulikwisha lakini Wizara ilishawaandikia barua kwa ajili ya kuleta mapendekezo katika hatua ile. Mpaka leo hawajatoa na limejitokeza hapa kama ni tatizo. Kwa hiyo, nawaomba sana Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa katika maeneo hayo watusaidie ili tuweze kutatua tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la uwezeshaji Mabaraza nalo limezungumzwa na Mheshimiwa Paresso tena, likazungumzwa na Mheshimiwa Makilagi, yamejirudia katika maeneo hayo. Mabaraza yana changamoto nyingi na ndiyo maana yamezungumzwa sana. Wengine wamezungumzia suala la kutoa elimu kwenye Mabaraza ya Kata. Napenda niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge kwamba suala la Mabaraza ya Kata yapo chini ya TAMISEMI. Kila tunapokwenda katika ziara tumekuwa tukishirikiana nao kuweza kutoa elimu katika yale mabaraza kwa kutumia wale Wasajili wetu wa Mabaraza kwenye yale maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishasema kwamba Halmashauri yoyote iliyopo tayari, Wizara ipo tayari kutoa wawezeshaji wakisaidiana na Mwanasheria wa Halmashauri kuweza kuwapa elimu wale Wajumbe wa Mabaraza waweze kufanya kazi yao vizuri. Hii ni kwa sababu haya yapo chini ya TAMISEMI, lakini kwa sababu yote yanasimamia Sekta ya Ardhi, basi tunashirikiana kuhakikisha tunawapa elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu lilizungumzwa na Waheshimiwa Wabunge hapa ni kwamba wapewe mafunzo ambayo imezungumzwa pia na Mheshimiwa Chumi, Mheshimiwa Bilakwate na Mheshimiwa Allan ili waweze kufanya kazi yao vizuri. Tutaendelea kusaidiana na Halmashauri zetu. Lengo letu ni kuhakikisha kwamba hawa watu wanapata elimu na wanawasimamia masuala yote ya ardhi katika maeneo yao kwa sababu wao ndio hasa waliopo kwenye zile changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Bunge lako hili, nawashukuru sana viongozi wa Mkoa wa Katavi na Sumbawanga, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya pamoja na Wakurugenzi, wamechukua hatua mahususi ya kuweza kuanza utaratibu wa kutoa mafunzo ya mabaraza hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Wilaya ya Kalambo walitoa mafunzo ya siku ya zaidi ya 20 kutaka kuwezesha yale Mabaraza. Jambo hili linawezekana pale ambapo dhamira ya dhati katika maeneo na viongozi husika wakiliona kwamba ni changamoto, inawezekana kuyapatia ufumbuzi. Nitumie fursa hii kuwapongeza na nitoe rai kwa mikoa mingine kuweza kuiga mikoa hii miwili ambayo imeweza kufanya kazi nzuri katika kuelimisha Wajumbe wa Mabaraza waweze kufanya kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbaraka Kitwana alikuwa anazungumzia mgogoro wa Shamba la Utumani lenye ukubwa wa hekari 4,000 na shauri hili lipo Mahakamani, kwa hiyo akataka sasa watu wa Mafia wafanyiwe ugawaji. Sasa nasema, hili suala bado halijafikia hatima yake. Kwa hiyo, haliwezi kufanyika jambo lolote katika utaratibu huo, lazima hatua za Kimahakama ziishe ili tuweze kwenda kwenye hatua nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Shangazi amezungumzia suala la Mnazi Sisal Estate la Lushoto ambalo nalo amelizungumzia. Taratibu za kufuta zimekwama kutokana na miliki za shamba hili kuwekwa dhamana benki. Hii ni kwa sababu kuna wamiliki wengi wa mashamba wengine walichukulia mikopo na hasa kwa Korogwe, Mkoa wa Tanga, mashamba mengi sana yamechukuliwa mikopo benki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo linapokuwa limewekwa dhamana ya benki, huwezi kuanza kufanya taratibu nyingine. Kasoro hizi ambazo zinatokana na hiyo, Halmashauri inaagizwa pia itume tena ilani katika shamba hilo ili benki waweze kupewa nakala ya ilani hiyo na ufutaji utaendelea baada ya taratibu zote kukamilika. Kwa sababu kuwa na dhamana isiwe ni kikwazo. Tumeni tena ilani na benki wapewe nakala ili wajue pamoja na kwamba wana dhamana hiyo, lakini shamba hili lina changamoto zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwakasaka alizungumzia suala la nyumba za NHC, watu kununua kwa wingi na kupangisha. Sina uhakika na malalamiko yake labda angetupa mfano mzuri ni wapi, kwa sababu Tabora, Uyui na Igunga kuna nyumba zimejengwa pale, hazijapata wapangaji na hazijanunuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa aliyenunua na kuhodhi nyingi ni zipi? Kwa sababu hiyo ni case study ambayo iko wazi kwamba nyumba zipo, lakini hazijanunuliwa. Ni vyema akatufahamisha ni wapi ambapo nyumba zimenunuliwa na mtu mmoja halafu anaanza kupangisha ili tuweze kuchukua hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lupembe vile vile amezungumzia nyumba ambazo zimejengwa lakini zinakaa idle. Niseme kwamba nyumba kukaa idle wakati mwingine Halmashauri pia zinakuwa zinahusika. Mnaomba kujengewa, zinajengwa. Zikishajengwa zimekamilika, hamko tayari kuchukua. Sasa hii kidogo inakuwa ni shida. Ndiyo maana tukasema, Mheshimiwa Kalanga alikuja na wazo la kwamba watu wapewe miaka mitano kulipa lakini Shirika la Nyumba linatoa miaka 10 kwa mpangaji mnunuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe maelekezo katika nyumba zilizojengwa ambazo Halmashauri hazijawa tayari kuzichukua, utaratibu wa shirika utabadilika kuliko kuacha ziharibike, zitakwenda kwenye ile sera ya mpangaji mnunuzi na zitauzwa kwa mtu yeyote aliyeko tayari kununua ili zile nyumba ziweze kupata wapangaji. Ikienda kwa mpangaji mnunuzi, maana yake una miaka kumi ya kuweza kulipa. Mheshimiwa Kalanga aliomba miaka mitano, lakini National Housing wameweka miaka 10. Kwa hiyo, bado nafasi tunayo ya kuweza kutumia nyumba hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, kwa sababu tusipofanya hivyo, haya mambo wakati mwingine tunaweza tukawa tunawalaumu wawekezaji, tunalaumu National Housing lakini sisi wenyewe tunaohitaji pia tunakwamisha. Niwape mfano mzuri wa Jimbo la Busokelo, waliomba wakajengewa nyumba nzuri za mfano na tayari wamechukua; na Jimbo la Momba pia nao wamejengewa nyumba nzuri na zinafanya kazi na wanakwenda hatua nyingine ya pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Halmashauri zetu, mnapohitaji muwe tayari pia kuhakikisha kwamba mnakwenda kuzichukua nyumba zile ili kuepusha uwekezaji unaokwenda kudumaa. National Housing hawawezi kusonga mbele kama wanawekeza halafu haziendi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Sakaya ameongelea wawekezaji wa miradi mbalimbali kwamba wapewe ardhi kuenenda na maeneo yanayofaa katika miradi husika. Viongozi wa Vijiji wapewe elimu. Hili tumelichukua kwa sababu Sheria ya Ardhi iko wazi na inatoa utaratibu mzima wa ugawaji ardhi. Sasa katika hili nadhani ni elimu tu izidi kutolewa kwa watu wetu waweze kujua ni jinsi gani ya kuweza kusimamia haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo la ujenzi holela ambalo limeongelewa na Mheshimiwa Kigola. Nadhani nimeliongelea kwa upana wakati nazungumzia masuala ya uandaaji wa mipango kabambe na kuhamasisha wananchi kutojenga ili kuepuka hili. Wizara inashirikiana na mamlaka za upangaji katika maeneo hayo ili kuandaa mipango kabambe na hili suala litakuwa limepungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Cosato Chumi ameongelea kupewa baadhi ya Watumishi nyumba za CDA. Wizara haihusiki moja kwa moja na utoaji wa nyumba hizi katika kupangia watumishi, lakini haya yamepokelewa na yanaweza kufanyiwa kazi kulingana na maombi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Watumishi wa CDA kutawanywa katika maeneo mengine, hili pia lipo chini ya Wizara husika kwa sababu CDA sasa hivi ipo chini ya Manispaa ya Dodoma, maana yake ipo chini ya Ofisi ya TAMISEMI. Hivyo, Wizara inayohusika kwa kushirikiana na Wizara yetu, kwa sababu wako pia Watumishi wengi tu wa Sekta ya Ardhi, basi tutaona ni jinsi gani bora ya kuweza kutatua hilo tatizo na hasa katika kuwapanga watu katika maeneo yanayotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani muda umekuwa finyu na mambo ni mengi. Naomba uniruhusu tu nizungumzie suala moja la asilimia 30 ambayo imezungumziwa. Ndugu zangu suala la asilimia 30 limezungumziwa na Waheshimiwa Wabunge nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudie tena; baada ya ile Sheria ya Bajeti mwaka 2016 tulivyoipitisha ya kuondoa mambo ya retention, asilimia 30 haipo tena. Ndiyo maana tulisema na nikipita katika ziara nawaambia kwamba Halmashauri zinazopanga bajeti ya asilimia 30 kutegemea Wizara, tunapotosha bajeti zetu, kwa sababu hiyo iliondolewa katika bajeti iliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa zinazokuja kwenye Halmashauri, zinatokana na OC ambayo Wizara inakuwa imepangiwa shilingi bilioni kumi kwa mwaka 2016/2017 kwa nchi nzima na zinatolewa kutegemeana na zinavyoingia. Kwa hiyo, haiji kama asilimia 30 ambayo wewe unaiweka. Kwa hiyo, unapoweka kwenye bajeti yako asilimia 30 kwamba unadai Wizara, kibajeti kidogo inakuwa haiko sahihi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nisisitize katika hili maana limekuwa likijirudia, hakuna asilimia 30 kama 30 inavyorudi kule. Kinachokuja ni OC kwa ajili ya kuziwezesha Halmashauri zetu kwa shughuli za sekta na pesa hizo lazima zifanye kazi ya Sekta ya Ardhi na siyo Mkurugenzi kupanga matumizi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, zitakuja kwa kadri zinavyoingia kutegemeana na bajeti ya Wizara iliyowekwa kuliko hiyo ambayo ninyi mnaitegemea sasa kwamba ni asilimia 30, inapotosha kila kitu katika maelezo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nawashukuru kwa kunisikiliza.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa ambayo tumeipata kuja angalau kujibu hoja za baadhi ya Wajumbe kwa maana ya Wabunge ambao wamechangia. Mpaka sasa waliochangia kwa kuongea ni 15 na waliochangia kwa maandishi ni 13.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuniamini, baada ya mabadiliko madogo ya Bazara la Mawaziri, basi aliendelea kuniacha katika Wizara hiyo ili niweze kuendelea kushirikiana na Mheshimiwa Lukuvi. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri wangu ambaye siku zote amekuwa akinielekeza na kuniongoza vyema katika kutenda kazi na tunawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wametupongeza kwa sababu tunafanya kazi kama team work kwa maana ya Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu pamoja na timu yake kule ndani. Pia kwa upande wa Waheshimiwa Wabunge tunashukuru Kamati ambayo imekuwa ikitusimamia na kutuelekeza vizuri. Napenda kuwashukuru pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitaishukuru familia yangu ambayo imenivumilia kwa muda wote pamoja na kufanya shughuli za Kitaifa lakini bado wameendelea kuniamini na kunivumilia. Nawashukuru wapiga kura wangu, muda wote tumekuwa nao na pale ambapo sipo nao basi wanaendelea kunivumilia kwa sababu walinipa dhamana na Mheshimiwa Rais akanipa dhamana nyingine ya Kitaifa, lakini wanalitambua hilo na nawashukuru sana na wengine wako hapa leo kushuhudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi zote zilizotolewa, nawashukuru sana Watendaji wetu wote katika Halmashauri, Manispaa, Majiji na Miji ambao wamebadilika sana katika utendaji kiasi kwamba wanafanya Wizara ionekane inafanya kazi vizuri, lakini ni kwa sababu ya uadilifu wao, wamekuwa wakizingatia yale ambayo tunaelekeza. Ni wachache tu ambao bado hawajakaa sawa, nasi tutaendelea kuwafuatilia ili tuweze kwenda nao sambamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nachukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kwa namna ambavyo anaendesha Serikali hii ya Awamu ya Tano katika maelekezo na mtazamo chanya wa kwenda kwenye uchumi wa kati, lakini pia tukiwa na kauli mbiu ya Tanzania ya Viwanda. Kwa kweli Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri wote tumelibeba hili kwa pamoja na tunahakikisha kwamba uchumi wa kati tutakwenda kuufikia na hasa tutakapotumia rasilimali ardhi vizuri kama ambavyo tunatarajiwa na watu waliotupa dhamana hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na michango yote iliyotolewa, katika kujibu hoja hizi tutazijibu chache kulingana na muda lakini nyingine zote tutazijibu kwa maandishi na Waheshimiwa Wabunge wote watapata nakala zao. Kwa uelewa wangu na nilivyoangalia maeneo mengi ambayo yamezungumziwa, tatizo kubwa liko kwenye uelewa ambapo wananchi wetu wengi hawajaweza kuelewa na ndiyo maana changamoto zinakuwa nyingi. Hawajajua haki zao na hawajajua wafuate utaratibu gani pale ambapo wanatakiwa kudai haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile uhaba wa vitendea kazi umezungumzwa. Haya yote yanachangia katika suala zima la kupunguza ufanisi katika maeneo yetu. Upungufu wa watumishi vile vile ni changamoto. Kwa hiyo, unapokuwa na mapengo kama hayo, lazima utendaji pia utakwenda kwa kusuasua kidogo kwa sababu ya uwezo mdogo katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ambazo zimetajwa na Wabunge na ambazo pia Kamati wamezungumzia, nitazijibu kama ifuatavyo kulingana na muda. Kamati yetu inayosimamia Wizara ya Ardhi, Maliasili na Utalii, wamezungumzia suala la pesa kutopelekwa katika Halmashauri zetu. Hili huchangia pia katika utendaji mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili tumelichukua na tunasema tutahakikisha kiasi kilichokuwa kimetengwa na wenzetu wa fedha hapa wanasikia, kitakwenda ili kurahisisha kazi za utendaji. Kwa sababu kama tuliwekea bajeti na pesa inakusanywa, basi kadri inavyoingia, ndivyo jinsi tunavyowapelekea ili waweze kufanya kazi zao. Kwa sababu wasipokuwa na rasilimali fedha hapo hapo na upungufu wa rasilimali watu lazima utendaji kidogo utayumba. Kwa hiyo, hili tumelichukua na tunatii maelekezo ya Kamati yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumziwa masuala mazima ya Shirika la Nyumba. Shirika la Nyumba limezungumziwa pia hata na wachangiaji waliochangia kwa kuongea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Shirika la Nyumba kama ambavyo sura ilikuwa inaonekana, sivyo ambavyo uhalisia wake ulivyo. Kamati inayosimamia imeshuhudia na imelizungumza pia katika taarifa zake. Napenda niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba Shirika letu la nyumba pamoja na kelele zilizoko nje, lakini bado lina uwezo wa kufanya kazi zake vizuri. Ukiangalia zile mali walizonazo, thamani yake inazidi shilingi trilioni 2.8 kwa maana ya thamani tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, madeni yaliyokuwa yanazungumziwa, shilingi bilioni 249, ukichukua thamani ya rasilimali ya majengo waliyonayo National Housing ukagawia kufanya hesabu ndogo tu, unakuta linaweza kuendesha au kulipa madeni yale mara ishirini zaidi kwa maana ya kwamba lina mtaji mkubwa hasa ukiangalia thamani ya majengo ukilinganisha na madeni ambayo wako nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapenda kuwahakikishia kwamba sura inayozungumzwa nje ni tofauti na uhalisia. Wajumbe wa Kamati wamefika na wameona. Kwa hiyo, napenda kuwahakikishia, changamoto nyingine zilizoko ndani, kwa mfano mmezungumzia suala la Menejimenti pengine, suala la bodi kutokuwepo, haya yote yanafanyiwa kazi na sasa hivi Wizara iko katika mchakato wa kuweza kuona kwamba ni jinsi gani tunaweza kupata bodi nyingine mpya baada ya Mheshimiwa Rais kuivunja ile nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua bila kuwa na bodi, kazi haziwezi kwenda vizuri. Kwa hiyo, hili kama Wizara linashughulikiwa kwa haraka na tutakwenda kupata taarifa siku siyo nyingi pale ambapo masuala ya vetting yatakuwa yamekamilika. Tukumbuke hili shirika ndiyo limebeba dhamana ya Wizara, ndiyo hasa ambalo tunatarajia liweze kumkomboa Mtanzania wa kawaida ukiacha haya mashirika mengine ambayo nayo yanafanya suala la uendelezaji miliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, tunahitaji Watanzania wawe na makazi bora na makazi ambayo yamepangika. Kwa hiyo, hili tumelibeba na tunalifanyia kazi kama ambavyo inatakikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lupembe amezungumzia suala la nyumba kuwepo na kwamba hazipati wanunuzi. Naomba niseme tu kwamba, katika suala zima la ujenzi wa nyumba, kuna Halmashauri ziliomba ikiwemo ile ya Mpanda kule Katavi, lakini kuna nyingine walijengewa baada ya National Housing kuweza kupata maeneo kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa zile Halmashauri ambazo ziliomba, basi zitekeleze malengo yake, kwa sababu, tumeshatoka kwenye kulazimisha kwamba watu lazima wanunue, suala la msingi sasa hivi, National Housing wana product tatu kwa maana ya kwamba unaweza ukawa mpangaji mnunuzi; unalipa kidogo kidogo baadaye nyumba inakuwa yako. Unaweza ukainunua moja kwa moja wewe mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haya yote yanawezekana, lakini kikubwa tunachotakiwa, pale ambapo Halmashauri inahitaji, tunaomba sana mikataba iwe kamili na muweze kumaliza gharama hizo na kuweza kuchukua zile nyumba. Nawapongeza wenzetu wa Uyui, ndiyo Halmashauri pekee inayoongoza kwa kununua nyumba nyingi ukilinganisha na Halmashauri nyingine, ikifuatiwa na wenzetu wa Busekelo, Mvomero, Geita na Halmashauri nyingine ambazo zimeweza kuchukua nyumba hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumziwa suala la manunuzi kwamba pengine utaratibu siyo mzuri. Naomba niwaambie, suala zima la manunuzi katika Shirika la Nyumba, linazingatia sheria zilizowekwa katika kumpata mnunuzi. Tuzingatie kwamba Shirika hili pia mbali na kuwa Shirika, lakini bado lina Taasisi mle ndani ambazo zimeandikishwa kisheria na zinatambulika. Zinapoingia kwenye mchakato wa kutaka kujenga, basi na wao wanatathiminiwa kama wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la kupata Wakandarasi linazingatia sheria na hakuna mahali ambapo panakiukwa. Kwa hiyo, hili tunalizingatia, tunalifuata na tunaheshimu ushauri wa Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imezungumzia suala la ukusanyaji wa mapato kuonekana kwamba pengine linasuasua na mapato hayapatikani. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu katika suala zima la ukusanyaji wa kodi ya pango la ardhi, aliweza kutoa fursa kwa wananchi ambao walikuwa wamelalamikia kwamba pengine wanapokwenda pamoja na tatizo la EFD Machines na mitandao katika Halmashauri zetu, walikuwa wanapanga foleni kubwa sana, wanashindwa kulipa kwa wakati. Akatoa miezi minne, lakini bado akaongeza mwezi huu wa Tano ambao unaokwenda kwisha kesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba muda ulioongezwa unatosha sana kwa wenzetu kuweza kutimiza wajibu wao kulipa kodi. Nami niseme kwamba baada ya kesho tunaomba sana Halmashauri zichangamkie fursa hii ya kuhakikisha kwamba inawabana wale wote ambao hawajaweza kuzingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto chache zinazoletwa na Wajumbe na Waheshimiwa Wabunge kwa kulalamika kwamba pengine gharama ni kubwa. Nadhani gharama siyo kubwa kiasi kile ambacho wanafikiria, lakini unapoona una changamoto kwenye invoice yako, tujue tatizo ni nini? Kwa sababu, suala la ardhi liko fixed, halipunguzwi wala halifanywi chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoweza kuangalia, ni lini wewe ulitakiwa kulipa na umelipa wakati gani? Kwa hiyo, interest inapigwa kila mwezi asilimia moja kulingana na wewe ulivyochelewa kulipa. Kwa hiyo, lazima tulione hili kwamba pia tunao wajibu wa kuzingatia muda wa kisheria ambao unatutaka kuweza kulipa madeni ambayo tunakuwa nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala zima la Mabaraza ya Ardhi ambayo yamezungumzwa. Nasema Mabaraza ya Ardhi mpaka sasa tunayo 97, lakini yanayofanya kazi ni 53, kwa maana ya kwamba yapo na Watendaji. Mpaka sasa hivi tuna kibali cha kupata Wenyeviti wa
Mabaraza 20 na tuna imani wakija hao wataweze kutupunguzia ile adha iliyokuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo tulilonalo, kila Mheshimiwa Mbunge akinyanyuka, akiongelea Baraza, kama haliko kwake, kama wana-share labda Wilaya mbili, anataka liende kwake. Naomba tutambue kwamba Baraza linakuwepo pale kulingana pia na idadi ya mashauri au kero zilizopo pale. Kwa sababu hata ukikuta kwamba Mwenyekiti anahudumia Mabaraza matatu au manne, kuna Baraza lingine unaweza kukuta kwa mwaka wana mashauri yasiyofika 200, lakini Mabaraza mengine unakuta kuna mashauri yanakwenda mpaka 1,000 na kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukikuta kwamba Mwenyekiti anakuja mara moja moja ni kutokana na wingi wa mashauri yaliyoko katika maeneo mengine ukilinganisha na ya kwako. Kwa hiyo, tunaomba tu tuvumiliane katika hili. Pia Wizara imetenga shilingi milioni 165 kwa ajili ya kufanya ukarabati katika maeneo mengine ambayo tunatarajia kuwa na Mabaraza. Kwa hiyo, nawaomba tu mvute subira kwa sababu tayari kama Wizara tumeshajipanga kuweza kuona ni jinsi gani tutaondoa hii adha ambayo imekuwepo katika suala zima la kuweza ku-solve matatizo ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie mipaka ambayo imezungumzwa katika suala zima la kulinda mipaka yetu. Wamezungumzia suala la usalama, hakuna ile njia ya kupita pengine kuweza kujua ni jinsi gani ambavyo unaweza ukalinda usalama wa mipaka yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kusema, kama tulivyojibu swali moja wakati limeulizwa hapa Bungeni, katika mkutano huu, tayari Wizara kwenye mradi pesa za maendeleo tulizokuwa tumeomba kwa mwaka huu wa fedha unaoisha, mlituidhinishia shilingi bilioni nne na tulizipata zote na kazi hiyo imeshaanza. Wanasafisha masuala ya mkuza ili ukae vizuri, kuweza kujua, mipaka ya nchi na nchi, lakini pia makubaliano ya kiasi gani kiachwe kutoka kwenye eneo la Nomad’s land kwenda kwenye eneo lingine, tayari wenzetu wa Uganda tulishaingia nao katika ile protocol kwamba ni mita 30. Zoezi la Kenya lilikuwa linaendelea. Upande ule wa Tunduma na Zambia kule tayari yalishazungumzwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa ambalo nataka kuwaambia ni kwamba, tunachohitaji kama Watanzania ni kuzingatia yale ambayo tumekubaliana kama nchi na nchi. Kwa upande wa Kenya na Tanzania bado kuna mazungumzo yanaendelea. Sasa suala la barabara ambayo itafanya kuwe na movement nzuri ya kuweza kukagua ule mpaka, hili linafanyiwa kazi. Tujue kwamba sekta ya barabara ni Wizara nyingine inayohusika lakini kwa sababu tunafanya kazi kama Serikali, tunalichukua na tunaenda kulifanyia kazi na tayari wenzetu ambao tulikwenda kukagua mipaka, tuliwaomba pia Halmashauri kwa sababu zile ni barabara za Halmashauri. Basi ihakikishwe angalau kunakuwa na upenyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inakosekana heshima ya nchi pale unapokwenda eneo, halafu ili uangalie mpaka wako lazima uingie nchi nyingine; na kama unapeperusha bendera, maana yake uishushe halafu uingie, ukitoka tena kule upandishe, inasumbua. Hilo tumeliona, tumepokea maoni ya Kamati linafanyiwa kazi na tunawaahidi litakwenda kufanyiwa kazi vizuri. Nawaomba tu wenzetu wa Halmashauri wajue yale pia ni maeneo ya usalama wao. Kwa hiyo, wanapochonga barabara zao, wazipe kipaumbele barabara za mipakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima limeongolewa la ukamilishaji wa maandalizi ya Sera ya Nyumba ya Taifa. Sera hiyo imefikia katika hatua nzuri. Sasa hivi tuko kwenye kukusanya maoni ya wadau. Pale ambapo tutakuwa tumeshakusanya wadau kuona wanaiboreshaje ile sera, italetwa hapa mtaweza kuiona, tutaendelea katika utaratibu wake wa kuandaa. Kwa sababu itapelekwa Wizarani kwa ajili ya ukamilishaji ili tuweze kujua, kwa sababu huwezi kutunga sera ambayo haihusishi wadau. Kwa hiyo, kama Wizara mnakuwa na draft ambayo mnaona kwamba sera itapendeza kama ikiingiza vitu fulani. Ili iboreshwe vizuri, ni lazima maoni ya wadau yaheshimike. Kwa hiyo, Sera ya Taifa ya Nyumba imeshafikia hatua ya kukusanya maoni kutoka kwa wadau mbalimbali na lengo likiwa ni kuiboresha. Itakapokuwa tayari, taarifa zitaletwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala limezungumzwa kuhusu tozo ya mwanzo kwa ajili ya kupata kiwanja (premium). Kweli watu wamepongeza na kusema ilitoka 15 ikaenda 7.5, ikaenda 2.5 na Kamati sasa imependekeza ishuke. Naomba kusema tu kwamba kama Wizara tulishaliona hilo na kadri unavyozidi kuwapa nafuu wananchi ndivyo jinsi kazi inavyozidi kuongezeka. Hata kazi ya urasimishaji iliyofanyika Mwanza mpaka kuongeza lengo, walipewa viwanja 35,000, lakini mpaka sasa wamevuka lengo wana 42,563 ni baada ya kupunguza kutoka 7.5 kwenda 2.5 ambapo Mheshimiwa Waziri ambaye ndio ana mamlaka hiyo aliweza kupunguza na kasi ikaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeipokea, kweli tumeona matokeo chanya pale ambapo unampa nafuu mlaji wa kawaida. Kwa hiyo, hili tumelichukua kama Wizara, tutaona namna bora ya kuweza kuhakikisha tunawapunguzia gharama wananchi wetu ili wengi waweze kumiliki maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai tu katika Halmashauri zetu, pale ambapo mnafanya zoezi la urasimishaji, zoezi hili siyo endelevu kama tunavyofikiri. Kwa ile miji ambayo imeshapanga mipango yake kabambe, pale ambapo mpango kabambe unaanza kutumika, unless uwe uliingiza wakati unapanga mpango wako kabambe, ukasema kutakuwa na sehemu kinaendelea na urasimishaji kama wenzetu wa Singida walivyofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haikuwa katika mpango huo, tunapoanza kutekeleza mpango kabambe maana yake zoezi la urasimishaji linakuwa halipo. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Halmashauri zote ambazo zina zoezi la urasimishaji na wakati huo huo bado kuna zoezi la master plan ambazo amekuwa anaziandaa, lazima kasi iongezeke na wananchi waelimishwe watambue kwamba unapokuwa unatekeleza mpango kabambe huwezi kuendelea kurasimisha kule ndani, utakuwa unagonganisha mambo ambayo siyo sahihi. Vinginevyo, vikiingiliana ina maana utakapokuja kupimiwa ni lazima uende sambamba na mpango kabambe ambao umeandaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai tu kwa Halmashauri zetu kuwaelewesha wananchi wetu waweze kujua. Maeneo yale lazima tuwaelimishe wananchi wetu waweze kupata namna bora ya kuwa uhakika wa milki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limeongelewa suala la migogoro katika vijiji vinavyopakana na hifadhi. Maeneo mengi yenye migogoro ya hifadhi, tunashukuru kwamba sasa kuna mradi ambao Idara yetu yetu ya Mpango wa Matumizi ya Ardhi inapofanya kazi pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa maana ya TANAPA wanakwenda kupima vijiji 392. Vijiji vyote vinavyozunguka maeneo hayo katika hizi mbuga ambazo ziko kama nane ambazo zinakwenda kufanyiwa kazi hiyo, jumla yake viko vijiji 427, lakini huu mpango ni wa kama miaka mitatu. Kwa hiyo, tunakwenda kupima maeneo hayo, yanapangiwa mpango wa matumizi bora ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani wakishafanya ile, hapatakuwa na kelele tena kwa sababu wananchi wenyewe wanashirikishwa. Hatua iliyoko sasa hivi ni kuelimisha wananchi namna ambavyo mpango huu utakwenda. Wameanzia ngazi ya Mkoa, Wilaya na baadaye watashuka kwenye vijiji vyenyewe ili viweze kushiriki. Hati zinazotolewa kule zinatambulika na mabenki. Tunayo mabenki zaidi ya 13 mpaka sasa yanatoa pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mmesikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri kipindi hiki, tayari zaidi ya shilingi bilioni moja zimetoka kwa kutumia hati miliki za kimila. Kwa mwaka wa fedha uliokwisha wa 2016/2017, mabenki yalishatoa pesa zaidi ya Sh.59,164,000,000/=. Kwa maana hiyo ni kwamba hati hizi zinatambulika na siyo kwamba hazitambuliki kama ambavyo wengine wanafikiria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nililiruka suala la Mheshimiwa Mtuka, ambapo aliongelea kuhusu mpango kabambe. Naomba kusema, maandalizi yoyote au mamlaka ya upangaji miji ni Halmashauri zenyewe husika. Kwa hiyo, Halmashari yoyote ikishaona kwamba sasa inahitaji kupanga mji wake vizuri, kuwa na mpango kabambe wa miaka 15, 20, wanatakiwa wao kuanza kuja na hoja yao, halafu Wizara itawasaidia pale watakapoona kwamba pengine wamekwama wanahitaji utalaam. Kwa hiyo, mchakato lazima uanzie kwenye Halmashauri husika kwa sababu ndizo zenye mamlaka ya kupanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba tu kupitia hoja ya Mheshimiwa Mtuka, maeneo ambayo pengine walitajarajia kuwa na mpango kabambe wanafikiri ni Wizara inayoanzisha, mnatakiwa wenyewe muanze, Wizara tunakuja kusaidia pale ambapo pengine mtahitaji utaalam, kwa sababu lazima pia Wizara ipitishe, utafika kwenye Wizara, utashauriwa pale panapohitaji kushauriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza miji ambayo tayari mipango yake kabambe imeshazinduliwa na inafanya kazi. Miji ya Musoma, Singida, Mtwara ambao wote wameshamaliza na kazi inaendelea. Mwanza na Arusha nayo iko katika utaratibu, wenzetu wa Dar es Salaam nao bado, mchakato nadhani haujakaa vizuri sana lakini, wako hatua hiyo. Tukishakuwa na hilo itatusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ILMIS ambalo mjumbe amepongeza, niseme tu kwamba Mheshimiwa Waziri wakati anawasilisha hotuba yake, ameongelea faida ya kuutumia mfumo huu na namna gani ambavyo tunaweza pia tukadhibiti wale watumishi ambao hawakuwa waadilifu sana, tukadhibiti masuala ya kuchakachua nyaraka kwa kumwagia chai, majani ya chai na nini. Ukishakuwa katika mfumo huu huwezi ku-temper nao hata mara moja. Kwa sababu kazi atakayeifanya mtu Wilayani, moja kwa moja Wizara inaona. Kwa hiyo, mpango huu umeanzia Kinondoni lakini utakwenda utasambaa kwa nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika hili tuelewe tu kwamba mfumo huu wa utunzaji wa kumbukumbu umeanza kwa majaribio, lakini utakwenda katika maeneo yote ili kuweza kuona ni jinsi gani ambavyo tunaweza kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la upungufu wa Watumishi katika maeneo yetu na vitendea kazi; naomba nimshukuru tena Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo amewarudisha Watendaji wa Halmashauri katika Wizara. Naomba niseme, kama Wizara tutakwenda kulisimamia hili, tutapitia watumishi wote wa sekta hii walioko kwa nchi nzima na kuweza kuwapanga katika utaratibu ambao uta-balance ili angalau kila Halmashauri iweze kuwa na uhakika wa kuwa na watumishi. Kwa sababu ni kweli kuna maeneo hawana Watumishi, kuna maeneo mengine hawana Watumishi wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili tutaangalia kwa upya tukishapata ikama yao wako kiasi gani na mahitaji ya kila Halmashauri then tuanze kuwapanga kwa uchache wao wakati huo tunaangalia namna bora ya kuweza kuongeza idadi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la vifaa vya upimaji kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameongea kwenye hotuba vitakuwepo by July. Nawapongeza sana, pamoja na kwamba na-declare interest kwamba mimi natoka Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, Ilemela wameweza kununua vifaa vyao wenyewe na vinawasaidia katika kasi ya upimaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tu Halmashauri nyingine, unapokuwa na vifaa vyako, unaepuka pia zile gharama ambazo zinakwenda kufanya gharama ya upimaji iwe kubwa. Kwa hiyo, pamoja na juhudi zinazofanywa na Wizara, pamoja na kuimarisha kanda zetu lakini bado pia kama Halmashauri tunahitaji kuona kipaumbele cha upimaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la fidia katika malipo, naomba sana na tumekuwa tukilizungumzia hili kwamba hatutakiwi kuwapunja wananchi; na mwananchi yoyote hataruhusiwa kutoa ardhi yake bila fidia, unless kuna suala ambalo ni la Kitaifa sana na halina mjadala katika suala hilo, bado kama Serikali tutazungumza nao na kuweza kuonesha umuhimu wa ule mradi ili aweze kuridhia. Ila hakuna kuchukua ardhi ya mtu bila kulipa fidia yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushuru sana kwa kunipa fursa ya kujibu machache. Kama nilivyosema, mengine tutajibu kwa maandishi, nimalizie tu kwa kuwashukuru wote na kuwatakia kila lililo jema katika Mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani, lakini pia tuombe ushirikiano wenu ambapo sifa zote mnazotupa hatuwezi kuzipata kama hatuna ushirikiano na ninyi. Nasi tunaahidi kuendelea kuwatumikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa hii ambayo tumeipata kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kuweza kuchangia hoja ya Wizara hii. Nianze kwa kuunga mkono hoja ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuniamini na kuniacha katika Wizara hii kuendelea kumsaidia katika majukumu ya utawala wa ardhi na shughuli nyingine zinazohusiana na ardhi. Nimshukuru Waziri wangu kwa maongozi yake mazuri, ni mentor mzuri kwa kweli anaweza kusimamia watendaji walioko chini yake na kuweza kuelekeza mambo yakafanyika vizuri na kweli tunafanya vizuri. Nimshukuru Katibu Mkuu pamoja na timu nzima yote ya Wizara pamoja na taasisi zilizoko chini ya Wizara, wanafanya kazi vizuri na tunashirikiana na ndio maana pongezi hizi zinakuja kwa sababu ya ushirikiano na namna ambavyo Wizara inasimamiwa.

Mheshimiwa Spika, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia. Tumepokea michango kwa maandishi kutoka kwa Waheshimiwa Waheshimiwa Wabunge 21 na Wabunge 17 wamechangia; kwa hiyo jumla ni 38; kwa hiyo tunawashukuru sana na pongezi zenu tumezipokea kwa sababu kazi kubwa tuliyoifanya tumeiona.

Mheshimiwa Spika, nisiwe mchoyo wa fadhila, niendelee kuwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Ilemela walioniamini na kunipa fursa hii. Nishukuru na watendaji wanaosimamia sekta hii wakiongozwa na Katibu Tawala Msaidizi wa Mkoa wa Mwanza ambaye leo anashuhudia hapa, yuko na maafisa kutoka Manispaa ya Ilemela pamoja na jiji kwa namna ambavyo wanafanya kazi nzuri na ndiyo maana pia mkoa unaonekana umefanya kazi vizuri kwa sababu ya usimamizi.

Mheshimiwa Spika, niishukuru familia yangu nikimshukuru na binti yangu mpendwa, Diana, leo amekuja kushuhudia; nashukuru sana kwa hayo.

Mheshimiwa Spika, napenda kuishukuru Kamati, kwa kweli ushauri walioutoa tumeuzingatia na tutaufanyia kazi. Kama ambavyo Wizara siku zote imekuwa sikivu. Kila wanapotupa ushauri ambao tunaona unajenga zaidi Wizara tunauchukua na tunaufanyia kazi; na kwa kweli kamati imekuwa ikifanya kazi kubwa ya kutoa ushauri pale ambapo tunaona kwamba tunahitaji oengine kuboresha zaidi, na wamekuwa wakifanya hivyo; na hata hotuba yao wameitoa ilikuwa pia, ina ushauri mzuri. Nimshukuru sana Mheshimiwa Mwenyekiti pamoja na kamati yake.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru Waziri Kivuli kwa hotuba yake nzuri, naye ametoa changamoto kadhaa na kuweza kutoa ushauri. tutayapitia yale yote ambayo ameyazungumza tuweze kuona namna bora ya kuweza kuyatumia yale yanayojenga; lakini nishukuru tu kwamba mmetambua kazi inayofanywa na Wizara na mpaka mkapongeza pia kwenye taarifa yenu. Kwa hiyo tunashukuru kwamba tunafanya kazi kwa pamoja, kwa sababu tunapojenga taifa moja tunahitaji kushikamana na kuhakikisha tunakwenda vizuri. Ardhi ni mali, ardhi ni mtaji; tusiposimamia vizuri kila mmoja atapata shida; si mpinzani si CCM si yeyote. Kwa hiyo tunashukuru sana pale ambapo tunakuwa tunazungumza lugha moja na inayoeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wachangiaji wamechangia mambo mengi, lakini kwenye upande wa mipango miji zaidi ya Wabunge 10 wamechangia na wote wakiongelea habari nzima ya namna ya kuweza kujizatiti katika kupanga makazi yetu yaliyo bora. Wengi wamezungumza, Mheshimiwa Kubenea amesema, Mheshimiwa Stanslaus Mabula, Mheshimiwa Aida Khenan, Mheshimiwa Mariam Kisangi, Mheshimiwa Mahmoud Jumaa, Mheshimiwa Charles Mwijage, Mheshimiwa Lwakatare, Mheshimiwa Mzava, Mheshimiwa Kamili, Mheshimiwa Selasini, wote wamechangia upande wa mipango miji.

Mheshimiwa Spika, napenda tu niseme kwamba, Wizara siku zote inajizatiti kuhakikisha kwamba miji yetu inapangwa vizuri. Ndiyo maana kama mlisikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri, tunayo miji zaidi ya 30 ambayo Master Plan zake zipo zimekamilika, kama Halmashauri 12 hivi, na nyingine ziko kwenye hatua nzuri ambayo tunakwenda; lengo ni kuhakikisha miji yetu inapangwa.

Mheshimiwa Spika, tatizo tunalokumbananalo tu ni kwamba staff tuliyonayo bado haitoshelezi kuweza kufanya kazi ile, na utaalam pia wa mipango miji unahitaji kuwa na timu ya wataalam inayoweza kufanya kazi ile kwa kasi kubwa na kuweza kufanya kazi inayokusudiwa; lakini lengo na dhamira ya Wizara ni kuhakikisha miji yetu imepangwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Stanslaus Mabula alizungumzia habari ya watu walioko milimani; na kama unavyojua Mji wa Mwanza una milima na kama ilivyo maeneo mengine kuna milima:-

Mheshimiwa Spika, kuna maeneo ambayo yalikuwa yameachwa kwenye suala zima la urasimishaji katika kupanga ile miji yetu. sasa lile eneo lilikuwa limeachwa kwa sababu jiji lenyewe lilikuwa na mipango ambayo walisema kwamba wao ndio wanatarajia mipango hiyo. Hata hivyo kwa hoja aliyoizungumza, ya kwamba tunahitaji pia kuwawezesha wale wananchi ili waweze kuwa na nguvu kiuchumi kwa kutumia rasilimali yao. Kwa sababu Halmashauri ya Jiji ina mpango wake leseni za makazi haziwezi kuzuia ule mpango kuwepo. Kwa hiyo, kwa hoja aliyoitoa kama Wizara tumeichukua, tutaona namna ya kuifanyia kazi vizuri ili wale wananchi ambao hawakupimiwa kipindi kile waweze kupimiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Selasini amezungumzia habari ya kukopesha halmashauri zetu ili ziweze kupima na kupanga. Niseme tu, ni juzi tu hapa tumetoa mikopo ya bilioni 6.2 hivi kwenda kwenda kwenye Halmashauri 24; na Halmashauri hizo zimepewa mkopo na masharti waliyopewa ni kwamba wahakikishe wanafanya upimaji vizuri, wanauza viwanja vyao na wanarejesha. Wakirejesha vizuri tunawapa tena; kadiri unavyokopa na kurejesha vizuri tunawapa kwa sababu tunajua hili suala la upangaji ni suala endelevu. Kwa hiyo, hiyo inafanyika na Wizara imeshalichukulia hatua vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika suala zima la upangaji tunapokuwa tunaendelea kupima kuna maeneo ambayo halmashauri zetu pia zinazungumza na wananchi kama kawaida, pale ambapo miji inakuwa imetangazwa kuwa iko chini ya mipango miji. Kuna namna wanavyokubaliana kiasilimia, utakuta Chemba wanakubaliana 60 kwa 40, ukienda kule Mkinga nao wamekubaliana; lile nalo linaharakisha zoezi la kupima kwa sababu unakuwa umeshawashirikisha moja kwa moja. Sasa kwa sababu hawana ile pesa ya kutoa moja kwa moja wanaridhia kutoa sehemu ya ardhi yao ili iwe ni pesa ya mchango kwao kwako wewe kuweza kuwapimia na kuweka miundombinu; na hili linafanika bila tatizo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi niseme tu, tutoe rai kwa halmashauri zetu waendelee kutumia mpango huu ambao tunaweza kusema ni barter trade, kwa sababu hela huna lakini ardhi unayo. Kwa hiyo unatoa kwa asilimia wanayokubaliana, wengine wana 70 kwa 30, wengine 60 kwa 40; lakini lengo letu ni kuhakikisha kuwa imepimwa. Wizara inachosema tu ni kwamba, haturuhusu kuchukua ardhi ya mwananchi bila kumlipa fidia, haturuhusu kuchukua ardhi ya mwananchi bila ridhaa na haturuhusu kuchuku ardhi ya mwananchi hlafu ukakaanayo bila kuiendeleza. Kwa hiyo hayo ndiyo maelekezo ya Wizara ambayo tunasema lazima yazingatiwe.

Mheshimiwa Spika, wamezungumzia suala la sera; kwa kweli ni jukumu la Wizara na tunakiri kwamba usimamizi wa sera na sheria katika Wizara ni jukumu letu la msingi katika kuhakikisha kwamba tunakuwa na sera ambazo katika utendaji zinatuongoza.

Mheshimiwa Spika, kama walivyosema, ni kweli Sera Nyumba, kama alivyoiongelea, kwamba inahitaji kuwepo; ni kweli na sisi tunaliona hilo lakini tayari mchakato ulikwishaanza, draft za mwanzo zilishafanyika na tulishaanza pia kupokea maoni. Kwa hiyo bado iko kwenye mchakato, itakapokuwa tayari tutaitoa kwa sababu tunaona ni pengo lililopo kweli, pasipokuwa na hiyo tunasema tunaposema tunataka kuwa na makazi bora, tunataka kuwa na nyumba bora, kama huna sera ambayo ipo itakuwa ni shida. Tunayo Sera ya Makazi ya 2000 lakini inahitaji maboresho fulani.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wakati anazungumzia ameongea kwa kina sana kuhisiana na hizi sera na mpaka aliongelea masuala ya real estate; ya kwamba tunahitaji pia kuwa na hiyo sera ambayo inasaidia sana katika kuhakikisha kwamba hawa waendelezaji milki hawajifanyii tu mambo yao jinsi wanavyojua. Ndiyo maana tunaona wengi wanajenga halafu na gharama na nini zinakuwa pia ni kubwa sana kulingana na hali halisi kwa sababu tu hicho chombo hakijawepo na kuweza kuwasimamia. Kwa hiyo hili kama Wizara tumelichukua na tunaendelea kulifanyia kazi kwa sababu tayari liko kwenye mchakato wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, wamezungumzia migogoro ya matumizi ya ardhi. Mheshimiwa Yussuf ameongea vizuri na ni Mjumbe wa Kamati, Mheshimiwa Abdala Mtolea amezungumza, Mheshimiwa Mndolwa ameongea katika haya katika masuala ambayo yanahusiana na migogoro hii.

Mheshimiwa Spika, ni wazi kumekuwepo na migogoro ya ardhi katika maeneo mengi lakini tumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa busara zake ambazo alizo nazo. Migogoro imekua ni mingi katika sekta mbalimbali, lakini Wizara zote za kisekta zimewekwa katika timu moja ambayo imepitia; na wakati Mheshimiwa Waziri anatoa hotuba yake pale alionesha kitabu kimoja kikubwa sana, kina migogoro ya kila aina mle ndani kulingana na sekta. Iko ya matatizo ya kwenye vyanzo vya maji, iko ya Jeshi la Wananchi na wananchi wenyewe, iko ya ardhi kwa wafugaji na wa kilimo, yaani iko ya aina nyingi. Kwa hiyo wamepitia mgogoro mmoja baada ya mwingine.

Mheshimiwa Spika, na hata kama hawakufika kwenye eneo lako, maana kuna baadhi ya Waheshimiwa Wabunge waliongea kwamba hawajafikiwa kwenye maeneo yao; lakini hatua iliyochukuliwa imegusa maeneo hayo, hata kama hawakufika unaweza ukakuta kwenye kitabu kipo kwa sababu wamehusishwa Wabunge. Ninyi wenyewe mlitoa migogoro pale ndani Mheshimiwa Waziri akawa anaipokea. Wakuu wa Mikoa walishakaa nao kila mkuu wa mkoa alipewa nafasi ya kuzungumzia wakatoa ile migogoro waliyonayo; lakini pia bado wananchi kwenye programu ya FUNGUKA NA WAZIRI wametoa. Kwa hiyo yale yote ambayo wameyakusanya sasa tunaangalia namna ya kuyapatia ufumbuzi kwa sababu ni jambo ambalo ni kubwa na linaingiza sekta nyingi. Kwa hiyo niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge tujaribu kuvumiliana katika hili ili tuweze kuona ni jinsi gani ambavyo tutaweza kulimaliza.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wameongelea suala la hati kutotoka. Kuna Mbunge mmoja amechangia kwa maandishi anasema hati hazitolewi. Kwa kweli, mimi nitashangaa kama tatizo hilo lipo kwa sababu Mheshimiwa Waziri hapa wakati anatoa hotuba yake ameonesha pia hata katika picha; zaidi ya hati 6,000 ziko kwa Dar-es-Salaam peke yake. Ukienda Mwanza kuna zaidi ya 2,000; nilikwenda pia Bagamoyo kule nikakuta kuna hati ziko pale zaidi ya 100, ziko tayari na watu hwachukui, zimeshalipiwa na hazidai. Hata hivyo kuna wengine ambao wameshapimiwa hawataki kuchukua hati kwa sababu wanaogopa watadaiwa.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme tu hili Waheshimiwa Wabunge kwamba kuanzia Julai 1, kama tunavyosema, yeyote ambaye amepimiwa ardhi yake, amelipia upimaji halafu hataki kuchukua hati kwa sababu tu atadaiwa kodi ya ardhi, maadam tayari ukishapanga na kupima umeshaingia kwenye system ambayo tayari tunajua kodi yako ni kiasi kadhaa na invoice unayopewa inaonesha kodi yako; tutaanza kuwadai wote, watalipa kodi ya ardhi uwe una hati hauna hati, maadam umepimiwa na tunajua wewe eneo lako ni hilo basi tutajua kwamba tutakudai. Tuwaombe sana ndugu zetu, kwa sababu tunasema ukikaa bila kuwa na hati ile ardhi yako haikusaidii. Huwezi kufanya shughuli zozote za kimaendeleo ambazo unaweza ukasema pengine uende benki upate mkopo ufanyie shughuli za kuweka dhamana mahali, hauwezi. Mimi nitoe rai tu kwa wananchi wote kwamba wafanye hiyo kazi ya kuhakikisha unakamilisha hatua nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Mheshimiwa mmoja amezungumzia habari ya upimaji kwenye urasimishaji kwamba watu wanalipa halafu hawapewi hati. Pia hapa kuna mambo mawili, kuna watu wanalipia upimaji halafu wanasahau kwamba hati inakuja kwa hesabu yake tofauti. Ile ya upimaji ni tofauti na ile unayolipia kwa hati. Kwa hiyo mimi niseme tunaendelea kuwaelimisha wananchi ili kwamba unapokuwa umelipia upimaji haina maana kwamba sasa unamilikishwa lazima pia gharama za kumilikishwa utapewa kwa sababu gharama za umilikishaji zinategemeana na ukubwa wa eneo, eneo mahali lilipo na matumizi ya eneo. Kwa hiyo haziwezi kuwa sawa, haziwezi kuwa flat rate kama hizi ambazo tunasema ni za upimaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na wakalalamikia kwamba, gharama za upimaji ni kubwa. Gharama za upimaji zinaweza kushuka kutoka hata hapo 150,000 ilipo kutegemeana tu na idadi ya viwanja na makubaliano. Tumekwenda nadhani Chemba wanadai kama 90,000/= nadhani, halafu Mkinga wana 60,000/=; kwa nini wengine wana-charge 60 wengine 150,000/=?

Mheshimiwa Spika, 150,000/= iliwekwa kama bench mark, kwamba haitakiwi izidi hapo, lakini inaweza ikashuka na kushukla kwake kunategemea pia na ile scope ya kazi anayokwenda kufanya. Kwa hiyo mimi niseme kuwa hayo yanawezekana; lakini pia halmashauri zinahimizwa kutumia vifaa vya ofisi ambavyo vipo vya upimaji, vinatolewa bure na hivi vinaongeza kasi, na watumishi walioko kwenye kanda wanayo nafasi ya kuja kwenye halmashauri zetu kuhakikisha kwamba wanasaidia katika zoezi la upimaji. Tukitumia fursa hiyo tuliyonayo hatutakuwa na tatizo katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wamezungumzia habari ya matatizo kwenye mabaraza ya ardhi na utendaji wa watumishi usioridhisha; na hii si kwenye mabaraza ya ardhi tu na katika ofisi nyingine za umma ambazo zimezungumziwa kwamba, usimamizi na utumishi wa sekta lazima uimarishwe kwa sababu, kuna watu wanakwenda ndivyo sivyo.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme tu kwamba, ikama ya watumishi kunzia Wizarani mpaka na taasisi zake bado iko chini. Wizarani tulitakiwa kuwa na watumishi 1,692 lakini tulionao ni 945 tu, maana yake tuna upungufu wa 747. Ukiena kwenye mabaraza tunao 173, lakini wanahitajika 844, tuna upungufu wa 671. Halmashauri 1,546 na walitakiwa kuwa 2,957 hivyo wana upungufu wa 1,411.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema kwenye hotuba yake, tunafanya upangaji upya wa watumishi katika Halmashauri zote ili kuhakikisha kwamba tunawapanga kulingana na mahitaji, tunawapanga kulingana na taaluma zao katika maeneo ambayo wanayo. Kwa hiyo niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwamba tuwe na subira haya yanafanyiwa kazi na tutaendelea kushirikiana pale ambapo tunahitaji kuboresha kutokana na michango mnayotupa.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naendelea kuunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumshukuru Mungu kwa fursa ambayo tumeipata leo hii kuweza kushiriki vizuri katika Bajeti yetu ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Aidha, imani huzaa Imani. Napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuniamini na kuendelea kunipa ridhaa ya kuwa katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana wananchi wote wa Jimbo la Ilemela ambao pia wameniwezesha kuingia katika Bunge lako hili kwa kipindi cha pili. Kwa uwakilishi, nawashukuru sana Waheshimiwa Madiwani ambao leo tuko nao hapa na wameshuhudia jinsi Mbunge wao anavyomenyeka hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru pia Waziri wangu kwa malezi mazuri katika Wizara, anatuelekeza na kutuongoza vyema. Sifa zote zinazosemwa hapa, zinatokana na uongozi shirikishi ndani ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana watumishi wote wa Wizara ya Ardhi kwa ushirikiano, pia nawashukuru sana Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hususan Kamati ambao wametupa ushirikiano mzuri sana katika kuhakikisha tunatenda kazi zetu vyema. Nakushukuru wewe pamoja na Spika na uongozi wote katika Bunge hili wakiwemo Wenyeviti kwa namna ambavyo tumeshirikiana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana viongozi wa dini ambao wameendelea kututia moyo kwa sala na dua zao, wanazidi kututia nguvu hata pale tunapokutana na magumu mengi yakiwemo ya magonjwa ya Covid na mengine, lakini wametuweka imara na tunaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho lakini siyo kwa umuhimu, naishukuru familia yangu, David na Sandra, Jacqueline na James, Diana na Emmanuel pamoja na Dorothy, kwa jinsi wanavyoweza kunivumilia katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kushukuru, basi nianze tena kwa kuwapongeza Wabunge wote waliochangia. Jumla ya Wabunge 33 wamechangia; 24 wamechangia kwa kuongea na tisa wameleta kwa maandishi, lakini pia kuna wengine wanane nilikuwa nimewasahau hapa, walichangia wakati ule wanachangia Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Hoja zao tumezichukua na wote waliochangia, hata kama sitaisema hapa na Waziri hataisema, tutazijibu kwa maandishi na tutawaletea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingi zinazozungumzwa zinatokana pia na uelewa pengine mdogo wa wananchi wetu lakini pia na lile suala zima la kutojua haki zao na wajibu wao katika suala zima la sekta hii ya ardhi. Hayo yote tutakwenda kuyafanyia kazi kutokana na miongozo mbalimbali ambayo tunaendelea kuitoa, elimu kupitia vipindi mbalimbali na vijarida tunavyovitoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze sasa kwa kujibu hoja ambazo ziko nyingi, nitajitahidi kadri nitakavyoweza. Kamati imetoa hoja nyingi, zaidi ya 30 ambazo wamezileta na sisi kama Wizara tumezipokea. Ya kwanza ilikuwa inaongelea habari ya Serikali kubuni mfumo endelevu ambao utahakikisha fedha za Serikali zinaletwa kutoka Serikali Kuu. Niseme ushauri umezingatiwa na ndiyo maana Wizara inaendelea kupata fedha na kuendelea katika kuweka kwenye vipaumbele ambavyo tumejiwekea. Kwa hiyo, zinakuja japo katika utaratibu ambao upo, unaeleweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuhusu Wizara kuelimisha wananchi, katika suala zima la ulipaji kodi, naomba niseme, Sheria ya Ardhi Na. 4 katika kile kifungu cha 33(1), kila mwananchi anayemiliki ardhi anao wajibu wa kulipa kodi ya pango la ardhi, lakini watu wanasubiri kusukumwa. Naomba tu Watanzania kwa ujumla tutii sheria, tuzingatie sheria zinasemaje? Kwa sababu mapato pengine yanapungua kwa sababu watu hatutii sheria zetu, lakini ukiangalia kile kifungu kinasema, “kila anayemiliki.”

Mheshimiwa Naibu Spika, pia mwaka 2020 hapa Wabunge wametupitishia mabadiliko ya sheria. Kifungu Na. 24A na Na. 33 kifungu cha 13 na cha 14, pale ambapo tayari upimaji unakamilika na surveys zinapita, tayari ana siku 90 tu yule mwananchi kuomba kumilikishwa. Asipomilikishwa ardhi ile, anaanza kutozwa kodi ya pango ya ardhi. Ile ni sheria ipo ambayo tunahitaji kuendelea kuwaelewesha wananchi ili waweze kujua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hili linafanyika, lakini watu wanapuuzia sheria. Nasi tumeshaelekeza, basi kwa sababu tayari Kamati imeona kuna upungufu katika makusanyo, lakini pengine inatokana na wananchi kutozingatia sheria, tutaendelea kukaza buti ili tuendelee pia kuhakikisha kwamba madeni yote au kodi zote zinalipwa. Mheshimiwa Hawa pia kazungumzia hili, nadhani yale yote yanayodaiwa kwa Serikali, yaani hayabagui; uwe ni ardhi uwe ni nani unadaiwa, lakini tunawadai fedha nyingi sana, ndiyo maana tunasema tutazidi kuzifuatilia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wamesema pia Wizara iagize wamiliki wote wa ardhi waingizwe kwenye mfumo. Tunaendelea kwa kutumia mfumo wetu unganishi wa ILMIS ambao sasa hivi unatumika kwa asilimia zote Dar es Salaam na mwaka huu wa fedha tunakwenda kuanza hapa Dodoma. Kwa hiyo pia itarahisisha kuweza kuwatambua wamiliki wote na kuweza kujua.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanaongelea pia Wizara kuandaa mikakati madhubuti ya kusimamia Maafisa Ardhi katika Halmashauri zetu. Naomba tuseme tu kwamba pamoja na kwamba Serikali imehuisha muundo wa ajira kwa Watumishi wa Sekta ya Ardhi na kuwaleta katika Wizara ya Ardhi kwa maana ya ajira pamoja na nidhamu, bado majukumu yao kama watendaji wako chini ya Halmashauri zetu. Kwa hiyo, ni jukumu la Halmashauri, hasa Wakurugenzi, kuhakikisha kwamba watumishi hawa wanawatumia katika kazi za upangaji, kupima na kumilikisha ili kasi iendelee kuwa vilevile. Kwa sababu kuletwa huku wengi wamekuwa pia wakijisahau, wanafikiri kwamba sasa wametolewa majukumu yao kwenye Halmashauri na wameletwa Wizarani. Wizarani tunasimamia suala zima la ajira na nidhamu, lakini kiutendaji, operational-wise ni a hundred percent wako chini ya Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, wamezungumzia suala la gawio stahiki kwa wakati liende kwenye Mamlaka za Mitaa. Naomba niseme tu, bahati nzuri Mheshimiwa Mabula amezungumza; retention ya 30 percent ilishaondolewa, na mliondoa hapa hapa Bungeni 2016/2017. Kwa hiyo, sasa hivi tunachofanya kama Wizara, ili kuzifanya Halmashauri zifanye kazi, ndiyo hiyo mikopo ambayo haina riba tunaipeleka na tumeendelea kutoa katika Halmashauri mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama taarifa mmeiona, tulitoa kwa Halmashauri 24. Pendekezo la Kamati linasema walau twende kwenye asilimia 50. Nasi tunasema tumelipokea kama Wizara na wenzetu wa fedha wanasikia kwa sababu tuko Serikali moja. Kwa hiyo tutaliona hili, kwa sababu tunajua huku ukiwekeza unakusanya pesa nyingi zaidi na kwa Halmashauri wanapata own source ya kutosha kutokana na pesa wanazopewa ambazo hazina riba, wanauza viwanja vingi na bado wanabaki na akiba ya kuweza kufanya maendelezo mengine. Kama ambavyo tumeona Mbeya, Ilemela, Kahama, Geita DC, Bariadi – wote haoa wamefanya. Wengine wamezitumia vizuri, baada ya kuwa wameuza viwanja wameweza kununua vitendea kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano Geita DC wamenunua gari; Mbeya wameongeza wigo wa kupima maeneo; Ilemela vivyo hivyo wameongeza wigo. Kwa hiyo, tutafanya kila jitihada kuhakikisha hili linatekelezeka ili tuziwezeshe kwanza Halmashauri zetu kwa kupanua wigo wa kipato cha ndani lakini pia kuhakikisha tunaongeza kasi ya upimaji. Hata hivyo, hii haiondoi wajibu au jukumu kubwa la Halmashauri la kupanga, kupima na kumilikisha. Sisi tunakwenda tu kama ku-support, tunafanya hizi interventions ili kufanya wigo wa upimaji uende kwa kasi na kupima maeneo mengi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna lingine limeongelewa kwamba Wizara ielekeze Halmashauri kupitia Ofisi ya TAMISEMI kutenga bajeti. Hatuielekezi TAMISEMI, isipokuwa tunafanya kazi kama Serikali kwa pamoja. Kwa hiyo, ni jukumu la Halmashauri kutenga bajeti zao na kuhakikisha kwamba hasa kupitia mapato ya ndani, watenge ili waweze kuongeza kasi katika suala zima hili la upimaji. Haya yote yanawezekana iwapo tutafanya kazi kwa kushirikiana ili kuongeza kasi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni Wizara kuzijengea uwezo Halmashari zetu. Kazi hii tumeshaianza. Kati ya hizo Halmashauri nadhani ni kama 184, tayari Halmashauri 102 tumeshazijengea uwezo wa kuweza kufanya kazi zake vizuri. Kwa hiyo, kazi tumeshaianza na tunaendelea, tutazifikia Halmashauri zote 184. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ya Kamati ilikuwa inasema Wizara iendelee kuwekeza nguvu kwenye kupanga na kupima. Nimeshalizungumzia, ambapo tunashirikiana nao kama Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala lingine linasema; kusimamia Halmashauri katika suala zima la marejesho ya mikopo iliyopewa. Katika hatua hii, naomba kwa dhati kabisa tushukuru Kamati zetu mbili, Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira pamoja na Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa na mikoa ambao wameweza kukaa kwa pamoja na kuweza kuyaunganisha majukumu haya na kuweza kuangalia kipi kinaweza kufanyika katika suala zima la ukusanyaji wa madeni? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ambacho tumekubaliana na tunaendelea kuweka mikakati ya pamoja ya kuweza kuona jinsi gani tutasimamia zoezi hili, ni kwamba wale wote wanaodaiwa waliitwa na walipewa taratibu za kulipa wakapewa muda, lakini bado sasa katika kuwapa Halmashauri nyingine tutaweka utaratibu kwa kushirikiana na TAMISEMI ili hata vile vigezo basi vifahamike. Siyo suala tu la kuandika labda proposal analeta halafu anapewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wengine wameandika proposals nzuri, na ndiyo hao wanadaiwa mpaka leo hawajaleta. Kwa hiyo, bado pia inahitaji kusimamiwa kwa karibu. Nami namshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya USEMI ambaye alizungumza kwamba hili wanalibeba na wanakwenda kulisimamia kwa nguvu zote ili waweze kwenda sambamba na hilo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kengele imeshapiga, lakini mambo yako mengi kweli. Ngoja nijaribu kuona nita-cover yapi, mengine itabidi tuwaletee kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, limeongelewa suala la National Housing hapa, hasa kwenye ule mradi wa Kawe ambao wanasema ni Kawe Seven Eleven, kwamba haujakamilika na pengine National Housing walipewa mkopo wakafikia ukomo sasa hawapewi tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, habari njema kwa Mbunge wa Kawe pamoja na Mbunge aliyeuliza swali, Mheshimiwa Halima Mdee, ni kwamba sasa hivi Serikali inafanya utaratibu wa kuweza kuwapa pesa waweze kumalizia mradi ule wa Kawe Seven Eleven. Pia Jengo la Morocco Square limeshafikia asilimia 94 ambapo ni uwekezaji mkubwa sana. Pale kuna vyumba zaidi 100 ambavyo vyote vinaingiza pesa, lakini kuna vyumba vingine katika mahoteli viko 80, kuna square meters 120,000 ambavyo vitawekewa maduka. Hivi vyote ni kitega uchumi kwa National Housing. Kwa hiyo, wakimaliza hiyo maana yake ni kwamba wataweza kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia alizungumzia suala la kutoingizwa kwenye bajeti. Suala la National Housing haliingizwi kwenye bajeti ya Wizara kwa sababu ile ni taasisi inayojitegemea, ina bajeti yake na haipati ruzuku kutoka Serikalini. Kwa hiyo, haiwezi kuwa sehemu ya bajeti ya Wizara ya Ardhi, isipokuwa Wizara ya Ardhi ni wasimamizi wa National Housing. Kwa hiyo, shughuli zote zinaofanyika, sisi kama Wizara lazima tuzisimamie na tuziripoti hapa kwenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Wabunge pia walitoa hoja zao kwa maandishi ambao sasa nitajibu kiasi kulingana na muda uliobaki. Wamezungumzia suala la ajira za kudumu kwa wenyeviti wa mabaraza. Ni kwamba Serikali kupitia Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa mwaka 2021, imewasilisha Mapendekezo ya Marekebisho ya Sheria ambayo yataleta utatuzi wa migogoro katika sheria hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, marekebisho haya yatarekebisha mfumo wa ajira kwa Wenyeviti wa Mabaraza kwa mikataba yao ile ya miaka mitatu mitatu waliyokuwa wanafanya. Sasa tunataka kuwaweka wawe kwenye ajira za kudumu ili wawe na confidence pia hata wanapofanya kazi zao. Kwa hiyo, hili tumelichukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la wazee kutolipwa na nini, nadhani kipindi kilichopita walikuwa chini ya idara nyingine, walikuwa chini ya Kamishna Msaidizi wa Mkoa, lakini sasa hivi wametengewa bajeti yao zaidi ya shilingi bilioni sita. Kwa hiyo, sasa hivi wana kasma yao ambayo inakwenda kuhudumia idara hiyo. Kwa hiyo, haitakuwa na shida tena kama ambavyo ilikuwa hapo mwanzoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala zima la mabaraza, kila Mbunge aliyechangia alisema habari ya kuwa kwake baraza halipo, ni Wilaya mpya. Tuseme tu kwamba ni mabaraza 111 ambayo yapo kati ya Wilaya karibu 139 ambazo zipo. Sheria inatutaka kila wilaya iwe na baraza lake, lakini Waziri alishaandikia Ma-RAS katika mikoa yote kuleta majina ya Wazee wa Baraza wa kila Wilaya ili wale wachache tulionao kabla hatujapata ajira ya wengine basi waweze kuwa wanakwenda kule kwenye maeneo kusikiliza kesi kwenye wilaya husika, badala ya watu kuja pengine anatoka labda Chemba au wapi kuja Dodoma, basi itabidi Mwenyekiti wa Baraza amfuate yule wa Chemba kule kule kwa sababu kutakuwa na Wazee wa Baraza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachoomba katika Halmashauri zetu na wilaya, waandae ofisi ambazo zitatumika kama mabaraza, kwa sababu sisi kama Wizara hatujengi, tunatumia majengo ya Serikali yaliyopo kwenye wilaya husika. Kwa hiyo, hilo nalo tutalitekeleza kwa namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, wamezungumzia suala la migogoro katika Jimbo la Newala ambalo limezungumzwa. Naomba niseme migogoro hii inashughulikiwa kwa kutumia Kamati ya Usalama ya Mkoa. Ni wazi kweli viongozi wa Newala hawakushirikishwa, lakini hata hivyo Wizara inajipanga kupitia watalaam wake kwa mwaka huu 2021 watakwenda kutatua suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, masuala ya madai ya fidia kwa Mamlaka ya Maji ya Masasi tuseme Wizara inaongea na mamlaka ile ili kuhakikisha hiyo fidia inalipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la Property Tax ambalo limezungumziwa ya kwamba nyumba zimejengwa ambazo pengine ni za watu masikini, lakini zinadaiwa Property Tax. Nataka tu niseme kwamba Wizara inafanya mawasiliano ya karibu na Ofisi zetu za TAMISEMI ambayo inaratibu kodi hiyo ya majengo ili kuona namna bora ya kushughulikia suala hili. Limeleta kelele kwa sababu hiyo kwamba watu wanaona ni kitu kipya, lakini kwa kawaida majengo yanalipiwa. Sasa ni majengo ya namna gani? Basi utaratibu unafanyika kuweza kujua ni jinsi gani tunaweza kuwafikia hawa na kuweza kuwadai wale wanaostahili.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, hoja zipo nyingi, lakini nashukuru tu. Baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Haya yote yaliyochangiwa tutayatolea maelezo kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni, nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri binafsi, Naibu Waziri na Watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba katika REA III vijiji 23 vifuatavyo vipatiwe umeme, ili waweze kwenda na kasi ya maendeleo sawa na maeneo mengine:-
Vijiji vya Lutongo, Kabusungu, Kilabela, Kilino, Isanzu, Igogwe, Shibula, Bulyanhulu, Ilalila, Chabakirua, Masemele, Igombe A, Igombe B, Mhonze A, Buganda, Zenze A, Zenze B, Iseni, Ilekako, Igalagale, Kasamwa, Imalang‟ombe na Isesa. Kazi mnayoifanya ni nzuri sana na inatia moyo, endeleeni kuchapa kazi msikatishwe tamaa na watu wasioitakia mema nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeambatanisha Shule za Sekondari zisizo na umeme. Naomba zipatiwe umeme maana ziko nje au vijijini; Mwinuko, Nundu, Kilimani, Shibula, Kirumba, Kabuhoro, Kangaye, Ibinza, Lukobe, Mihama na Sangabuye.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja. Aidha, niwapongeze sana Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya pamoja na kuwa na changamoto nyingi, Mungu mweza wa yote awatie nguvu, mtende kazi bila kuchoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni tamaduni za makabila; niwaombe katika suala la utalii muangalie pia historia na tamaduni za makabila mbalimbali kwani chaweza kuwa kivutio kikubwa cha utalii, kupata historia na utamaduni wa makabila husika. Mfano Kituo cha Bujora na Kayenze Mkoa wa Mwanza, kwa Wanyamwezi Tabora (Mwinamila), tamaduni na historia za Mkoa wa Kagera, Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Iringa na Mkoa wa Ruvuma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Makumbusho ya Mkwawa - Iringa, kuna mengi ya kuvutia watalii, lakini pamesahaulika sana. Historia ya Mkwawa hakuna asiyeifahamu lakini kituo chake kimesahulika sana na pamechakaa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fidia kwa waathirka wa kung‟atwa na fisi; Jimboni kwangu katika Kata ya Sangabuye na Bugogwa zaidi ya watu nane waling‟atwa na fisi na wawili hali zao zilikuwa mbaya sana. Halmashauri italeta madai ya wananchi wakidai fidia kwa madhara waliyoyapata. Vilevile kwa habari nilizopewa, ninaomba walete ushahidi wao baadhi yao walipwe fidia siku za nyuma. Ninaomba mara watakapoleta madai yao yashughulikiwe mapema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wafugaji na wakulima; ni vyema kama ambavyo imesemwa mara nyingi na Wizara yetu imelizungumzia, tupange kukutana na Wizara zinazohusika ili tumalize kero hii, watu wawe wafugaji wasiosumbuliwa. Iwapo kuna haja ya kumega maeneo ambayo yamevamiwa na makazi ya watu, tupime uzito ili kuondoa kero na kelele za mara kwa mara. Lengo la Serikali ni kuondoa kero, lakini kuwafanya wananchi waheshimiu sheria za nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu liwe endelevu ili watambue mipaka yao, zaidi sana wawe sehemu ya kulinda mazingira na hifadhi zetu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. DR. ANGELINA S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja. Ombi langu wananchi wa Kata ya Kanyerere na Kata jirani katika Wilaya ya Magu wana tatizo kubwa la usafiri kuweza kufikia visiwa vya base (Ilemela) na kisiwa cha Mashoka – Magu. Katika Kikao cha RCC kilichofanyika Mkoa wa Mwanza Januari, 2017, waliahidi kupeleka kivuko baada ya kufanya tathmini ya abiria, mizigo na shughuli za kiuchumi zinazofanyika katika visiwa hivyo na kuona vinastahili kuwa na kivuko. Ombi langu ni utekelezaji wa ahadi hiyo.

(1) Barabara ya Sabasaba - Kiseke hadi Buswelu ilikuwa ahadi ya Waziri alipotembelea Jimbo langu, naomba barabara hiyo kuwa ni kiungo cha Makao Makuu ya Wilaya na Kata zaidi ya saba ijengwe. Aidha, barabara hiyo itarahisisha pia kuwa kama mchepuko wa wasafiri waendao Mara na Shinyanga.
(2) Barabara ya Airport, Kayenze hadi Nyanguge nayo pia itasaidia mchepuo kuelekea Mara na Serengeti katika Mbuga za Wanyama na kuchochea utalii katika maeneo hayo.
(3) Tunahitaji minara ya simu katika Kata ya Kayenze na Sangabuye hawana mawasiliano ya uhakika katika baadhi ya mitaa ya Kata hizo za Kabusungu, Igumamoyo, Imalang’ombe na kadhalika.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. ANGELINA S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha niwapongeze sana kwa kazi nzuri mnayoifanya katika Wizara hii kwa kushirikiana na Naibu Waziri na timu nzima ya wataalam. Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki muendelee kuwatumikia Watanzania. Vilevile nichukue fursa hii kutoa shukrani kwa mara nyingine kwa mgao wa gari la wagonjwa, hakika mlitusaidia kwa kiasi kikubwa sana kusaidia huduma ya mama na mtoto katika jimbo langu hususan Kituo cha Afya Sangabuya ambako gari lilipelekwa na Kituo cha Afya Karume linakotumika pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni kwamba Manispaa ya Ilemela haina Hospitali ya Wilaya mpaka sasa, kwa juhudi za Halmashauri na kwa msaada wa Serikali Kuu jengo la wagonjwa wa nje tayari limepanuliwa. Tunaomba Wizara isaidie ukamilishaji wa hospitali hiyo ili kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando na Hospitali ya Mkoa ya Sekou Toure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Manispaa ina vituo vya afya vitatu tu kati ya 19 vinavyotakiwa. Pamoja na mapungufu hayo, vituo tulivyonavyo bado vina mapungufu mengi sana. Naomba Wizara yako katika majengo ya theatre yatakayojengwa nchini walau kituo kimoja kipate, hasa kituo cha Buzuruga ambacho kina mapungufu mengi. Kwa kuainisha Kituo cha Afya Buzuruga, kinahudumia wagonjwa takribani 25,877 lakini hakina jengo la upasuaji, wodi ya wanaume wala wodi ya akina mama waliojifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Karume kinahudumia wagonjwa 25,654 lakini hakuna nyumba za watumishi pamoja na jengo la wagonjwa wa nje. Kituo cha Afya cha Sangabuye hakina nyumba za watumishi, hakuna wodi ya watoto, hakuna wodi ya wanaume. Tunaomba walau tupate jengo la wodi kwa wanaume na watoto.

MheshimiwaMwenyekiti, tuna upungufu mkubwa wa watumishi katika kada ya wateknolojia maabara, wateknolojia dawa, wahudumu wa afya pamoja na watunza kumbukumbu za afya.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie katika Mpango huu. Nianze kwa kuupongeza mpango pia niseme tu tunapokea maoni na ushauri wa Wabunge ambao wameutoa japokuwa hapo baadae nitatoa ufafanuzi kwa kufafanua baadhi ya mambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba Wizara ya Ardhi ni Wizara wezeshi, na Mpango wa Maendeleo unaozungumzwa katika suala zima la uwekezaji hususani kwenye miundombinu Wizara ya Ardhi inayo mchango mkubwa kuhakikisha kwamba inaweka mazingira mazuri ili kuweza kuona mpango huo unakwenda vizuri.

Mheshimwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha huu ambao tunaendelea na tutakaokwenda kuendelea nao mwaka ujao, tunao ule mradi wa kuimarisha miondombinu kwa ajili ya upimaji. Tunatambua nchi imepimwa kwa asilimia isiyozidi 30 ni kama asilimia 25. Kwa hiyo kwa sasa tunazo pesa zile ambazo ni Dola za Kimarekani milioni 65 ambazo zitatumika kuimarisha miundombinu ya upimaji na tutakwenda kupima nchi walau katika sehemu kubwa. Lakini pia kuna ile ya uboreshaji milki, ambazo ni Dola za Kimarekani milioni 150. Kwa hiyo ukikamilisha maeneo hayo maana yake tutakuwa na zile base map ambazo zitakuwa zinatupa picha ya kuweza kupanga matumizi ya maeneo katika nchi nzima ikiwemo na hiyo miradi ya kimkakati ambayo tunayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika uchangiaji jana Mheshimiwa Mbunge wakati anachangia ilionesha kwamba pengine maamuzi ya Serikali ya eneo la Mbarali yangeweza kufifisa matarajio ya Watanzania pengine katika suala zima la kuichumi. Naomba kwanza niwatoe wasiwasi wananchi kwamba, mpango ule ambao umewekwa na Serikali ikiwemo hiyo ya mabwawa kama alivyosema Waziri wa Kilimo uko pale pale na mabwawa yale yapo mbali na eneo ambalo wananchi wameondolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile maeneo yale ambayo wananchi wameondolewa ni vijiji vitano na si vijijini 48 kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge alisema. Vijiji hivyo vitano vinavyoondolewa tayari elimu imeanza kutolewa ambapo maendeleo yanaenda vizuri na wanaweka alama kuhusiana na wapi wanaishia. Lengo letu ni kuhifadhi lile eneo ili maji yaendelee kutiririka katika Mto Ruaha ambayo yanapeleka kwenye Bwawa la Mwalimu la Nyerere. Kwa hiyo tukiharibu miundombinu ya pale maana yake ni kwamba tutajikuta tumeharibu mkakati mzima wa kuwa na umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo suala la kusema kwamba pengine labda tuanaondoa uchumi wa wananchi, tunaimarisha uchumi wa wananchi kwa kuwa na miundombinu ya uhakika itakayotuma umeme wa uhakika na uzalishaji utakuwa ni mzuri…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri kuna taarifa, Mheshimiwa Sanga.

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafuatilia majibu ya Mheshimiwa Waziri. Katika miradi 54 ambayo yamesaini kuna maeneo mawili ambayo wananchi wanaondolewa na miradi inaenda kujengwa. Moja ya eneo hilo linaitwa Mwendamtitu wanaenda kujenga mradi wa umwagiliaji na wananchi wanaondolea. Eneo la pili linaitwa Madibila Phase II wanaenda kujenga mradi wa umwagiliaji na wananchi wanaondolewa. Katika maeneo hayo wanayowaondowa Serikali imeshapeleka combined harvest machine 15 kwa ajili ya wananchi hao ili waweze kuendelea kulima, lakini kwa ripoti ya Mheshimiwa Waziri nampa taarifa kwamba hata dakika hii ninavyozungumza wananchi wanaweka beacon kwenye maeneo hayo ili wananchi waondoke na hawana taarifa na hawajashirikishwa.

MWENYEKITI: Kwa sababu Waziri ametaja idadi ya vijiji, kasema ni vijiji vitano na si 48 hivi vijiji unavyovitaja wewe viwili, vipo katika vitano ambavyo Waziri hajavitaja, vinavyoondolewa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu hajataja majina ya hivyo vijiji, kwa hiyo sijajua ni vijiji gani anavyovitaja lakini ninavyotaja mimi, ni hivi vijiji vya…

MWENYEKITI: Labda hivyo vipo kwenye yale mengine. Mheshimiwa Waziri vijiji vitano vinanavyoondolewa haya mawili sijajua kama unayo ile orodha ya hivyo vijiji vitano ama hauna tunaweza kupata taarifa baadae.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo taarifa yote ya vijiji vinavyobaki ambavyo ni kumi na tano, vijiji vinavyoondolewa ni vitano. Halafu…

MWENYEKITI: Sawa sasa hebu tusaidie hivyo vijiji vitano, hivi viwili anavyovitaja Mheshimiwa Mbunge hapa vimo katika hivyo vitanno au havimo.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vinavyoondolewa ni kijiji cha Luhanga, Madundasi, Msanga, Iyala na Kilambo. Mabwawa yanayokwenda kujengwa katika eneo lile katika Wilaya ya Mbarali, mabwawa yaliyotajwa yanajengwa na umbali wa bwawa ambapo yapo hayako kwenye yale maeneo ambayo wananchi wanaondolewa. Tunalo bwawa mmoja Scheme ya Msesule liko kilometa tano kutoka pale ambapo wananchi wanatolewa, tunayo scheme ya Utoro na Scheme ya umwagiliaji ya Isenyela ziko kilometa 11 kutoka pale mwananchi wanapotolewa. Tunayo Scheme ya Chozi na Scheme ya umwagiliaji ya Heman iko kilometa 30 kutoka pale wananchi wanapotolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokisema hapa, lengo la Serikali inachofanya ni kutaka kuweka mazingira mazuri kwa miradi ya kimkakati ambayo ndiyo inakwenda kukuza uchumi, moja wapo ikiwa ni hilo bwawa la Mwalimu Nyerere.

MWENYEKITI: Mimi nimekuelewa Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Mbunge ulikuwa unatoa taarifa, hivyo vijiji vilivyotajwa kuondoka, Mheshimiwa Waziri amevitaja, hizo scheme mbili ulizotaja zipo katika vile vijiji vitano au ni nje kwa kuwa ulikuwa hujamsikia bado Waziri.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, vipo kwenye hivyo vijiji vitano kwenye Mwendamtitu na Madibila phase II.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri wa Kilimo hizo scheme zipo upande gani? Hizo scheme mbili alizozitaja.

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Scheme ya Madibila Phase II, Phase I imekamilika, Phase II kuna kipande ambacho kinaingia kwenye GN 28 siyo Phase II 100 percent. Kuna kipande kinachoingia ndani ya GN 28. Tunachokifanya ni kwamba wakati technical team inaendelea kule ground na sisi ndani ya Serikali tunaendelea kufanya consultation. Kwa hiyo nimwambie…

MWENYEKITI: Haya hiyo ni nini? Mbarali nini, Madiba Phase two, hiyo scheme nyingine Mheshimiwa Waziri.

MHE. FESTO R. SANGA: Hiyo scheme nyingine ipo Mwendamtitu.

MWENYEKITI: Haya Mwendamtitu? Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, imo au haimo?

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika scheme ambayo inayoathirika ni Madibila phase II tu.

MWENYEKITI: Pekee yake?

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, yes.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri wa Ardhi.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa kutoa ufafanuzi pia. Zoezi ambalo linaendelea sasa hivi ni kuonesha mipaka kwa sababu kilio cha wananchi wa Mbarali alichokuwa anakisema walikuwa wanalamamikia GN Namba 28. GN namba 28 iliwekwa 2008 kwa Muswada ambao ulipitishwa hapa na baadaye ukaridhiwa na Mheshimiwa Rais kwa ajili ya ku - protect yale maeneo ya hifadhi ambayo yanapeleka Maji Mto Ruaha na unaokwenda mpaka Mtera pamoja na Kidatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kile kinachofanyika pale sasa hivi ni kuhakikisha kwamba, mpaka unaainishwa ili maeneo yale ambayo yanatunza vyanzo vya maji na mapokeo, ile catchemet area yote ya maji, iweze kubaki wazi na kurudisha ecolojia ya pale ili miradi tunayokwenda nayo isije kuwa imevuruga yote. Kwa sababu tunatambua pia uhifadhi hauruhusu shughuli za kibinadamu; tukiruhusu maana yake tunakwenda kuharibu pia ile hifadhi ya Mto Ruaha.

MHE. BONIPHANCE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. BONIPHANCE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mimi nataka kuiona hii dhana ya kusema sawa tunatunza vyanzo vya maji kwenye eneo. Hivi tatizo la Mto Ruaha kuisha maji, ni kwamba maji hayaendi mtoni au ni kwamba ule mto umekuwa tambarare maji yote yakienda yanapita yote. Lazima hili nalo tulione, Kwa sababu maji yanaweza kuingia masaa yote ya mvua lakini yakaondoka yote yakaenda ziwani. Tutafute alternative nyingine ya kuweza kuzuia maji kwenye Mto Ruaha. (Kicheko)

MWENYEKITI: Nadhani alikuwa anachangia zaidi kuliko kukupa taarifa, Mheshimiwa Waziri, malizia mchango wako.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza pamoja na mchango wake lakini majibu anayo pia. Kwa sababu unapofanya shughuli za kibinadamu karibu na eneo la hifadhi ya mto maana yake yale maporoko zile siltation inayofanyika inakwenda kuondoa kina cha maji. Matokeo yake…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki anachokizungumza, kwamba maji ya Mto Ruaha yamekauka kutokana na shughuli za wale wananchi wanaolima pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kutoa taarifa, wananchi wanaolima lile eneo linaloondolewa ambalo ni hekta 53,000, wanalima kati ya mwezi wa kumi na mbili, wa kwanza hadi wa nne na watano. Yale maji hayachepushwi kuingia mashambani kwa wakulima, lakini ni estate mbili ambazo ni za mwekezaji na sisi tunaungana nao wale wawekezaji, ndio wanaotumia maji yanayotoka kwenye Mto Ruaha kwenda estate zao. Kwa hiyo, si wale wakulima wanaotumia wao maji. Wanatakiwa mlifahamu hilo.

MWENYEKITI: Sawa, umeeleweka. Mheshimiwa Waziri hajasema wale ndio wanaokausha maji. Sijamsikia akisema maneno hayo, kwamba shughuli zile ndizo zinakausha maji ila alikuwa anaendelea na sentensi kwamba ukifanya shughuli za kibinadamu kwenye maeneo ya vyanzo. Sasa alikuwa anaendelea kwa sababu alikuwa anamjibu Mheshimiwa Getere. Kwa hiyo alikuwa hajamaliza hoja yake ni nini kwenye hili. Kwa hiyo nampa nafasi Mheshimiwa Waziri, endelea.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kutoa ufafanuzi ni wazi ni kweli nilkuwa naendelea moja wapo nimesema ni kufanya shughuli za kibinadamu. Pia ule uharibifu mkubwa wa mazingira uliopo katika maeneo yale ndicho chanzo pia kwanza cha kukosekana mvua ya uhakika ambayo inaweza ikapeleka maji katika yale maeneo. Kwa hiyo kile kitu kinachofanyika pale kinafanya pia hata mtiririko mzima wa maji, vile vijito vinavyopeleka maji kwenye Mto Ruaha navyo vinakauka. Maana yake ni kwamba hatima yake kutakuwa na ukame ambao hautaweza kurejesha tena ekolojia ya pale jinsi ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe mwenyewe unafahamu, historia ya eneo lile namna ambavyo Tume na Kamati mbalimbali …

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume na Kamati mbalimbali zikiwemo hata na Kamati za Bunge, zimekwenda na majibu yao yalikuwa ni yale mapendekezo ya kutaka kuhakikisha kwamba shughuli za kibinadamu pale zinasimama ili kulinda mazingira yale na kulinda hifadhi ambayo tulikuwa nayo kama uchumi wa Taifa letu unavyotegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kusema hayo. Lakini katika eneo hilo pia si wote wanaondolewa kuna vijiji 15 kama nilivyosema vinabaki na vingine 14 ni baadhi ya vitongoji. Unaweza ukakuta kwenye kijiji kitongoji kimoja na nilitaja vyote na orodha ninayo hapa, wakihitaji tunaweza kuwapa. (Kicheko)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii kuweza kutoa machache kulingana na Taarifa ya Kamati na niishukuru pia Kamati kwa hoja zao na mapendekezo waliyoyatoa na niishukuru kwa ushirikiano wao ambao wamekuwa wakituonesha, wakitupa kama Wizara, ushauri na maoni yao mara nyingi tunauzingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda mbali naomba tu pengine kwa wazo la ujumla katika taarifa ya Kamati mwanzoni wakati anaongelea habari ya Wizara kulikuwa na maazimio sita ambayo yanasema hakuna hata moja pengine ambalo limefanywa kwa ukamilifu. Pengine Kamati na Mwenyekiti utanisadia; moja ya azimio lililokuwepo lilikuwa ni lile la Bodi pamoja na Mabaraza yanayoshughulika na usijali, basi yashughulikie nidhamu za watumishi na wataalam pale wanapokuwa wanaharibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tumelijibu kwa ukamilifu kabisa kwamba hatua zimeshachukuliwa kwenye Bodi ya Udhamini, masuala kumi yameshughulikiwa kati ya hayo makampuni matano yamelipishwa faini, kampuni moja imesitishiwa leseni na wataalam watatu wamepewa onyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda upande wa usajili wa wataalam wa mipango miji, masuala kumi na tano yameshughulikiwa, ambapo wataalam nane wamepewa onyo, wataalam watatu wametozwa faini, kampuni tano zimesimamishwa kufanya kazi na kampuni mbili zinatarajiwa kufikishwa mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Baraza la Taifa la Wapima kuna maonyo pale yametoka manne, lakini Kampuni tano zimefutiwa leseni. Sasa pengine labda ule ukamilifu wa kutekelezwa ni upi, pengine watanisaidia labda sikuweza kueleawa vizuri, lakini tumeyafanya kwa ukamilifu kama ambavyo maazimio yalikuwa yanasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hili suala la Mradi wa Uboreshaji wa Milki ambao Wajumbe wamelizungumza na Kamati pia imelisema katika azimio lake, na ndiyo maana pale nikatoa taarifa ya kwamba unapoanzisha mradi wowote unakuwa na malengo, na lengo kuu la mradi huu kama nilivyosema naomba niisome kama ilivyo nisije nikaikosea.

Lengo kuu la mradi ni kuweka miundombinu ya kujenga mifumo, kujenga uwezo wa wataalam na kununua vitendea kazi ili kuwezesha kazi za upangaji, upimaji, umilikishaji kuwa endelevu ikiwemo upimaji wa mipaka ya vijiji na uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi. Huwezi kwenda kupima vijiji tu peke yake kabla ujaweka ile mipango, kama huna miundombinu huwezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imezungumzia suala la kwamba mifumo ipo katika mikoa miwili na haifanyi vizuri sana na hasa ya Dodoma. Sasa mradi huu unakwenda kuweka mifumo kwa nchi nzima mikoa yote, maana yake ni kwa wataalam wetu sasa kote watakwenda kufanya kazi hii na ule mradi wa kufanya data conversion tumeshakamilisha ramani zote za ardhi na ramani zote za mipango miji kwa asilimia 100. Kinachofuata sasa ni mifumo ili kazi hii iende kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mbali na hiyo mradi huu unakwenda kwenye Mikoa 16, Halmashauri 41; kati ya hizo Halmashauri 41, Halmashauri 34 zinakwenda kutoa hatimiliki milioni moja na kwenda kutoa leseni za makazi milioni moja; halafu Halmashauri saba zinaenda kupimiwa vijiji 250; sasa hii pesa inazungumzwa kama vile inaenda kufanya kazi moja wakati ina kazi nyingi tofauti na ambavyo wanavyofikiria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti, kwenye mradi wenyewe kama ulivyo ukienda kwenye kile kipengele cha tatu ambacho ndiyo kinajumuisha kama miundombinu, ukienda unangalia mradi mmoja baada ya mwingine kipengele kimoja baada ya kingine kila moja ina kazi ambayo ni compliment ya kile kinachoenda kufanyika finally. Huwezi kwenda kutoa hati tu kabla hujafanya maandalizi mengine. Hati ni final product baada ya haya mengine yote yamekuwa yamefanyika. Upimaji unakuwa umefanyika na kila kitu kinakwenda, ukiangalia hapa wanapozungumza ofisi 25 kwa mikoa yote zinaenda kujengwa na ile mifumo sasa ya muunganiko wa taarifa za wamiliki wa ardhi zinakwenda kuingia katika ile mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia pia kuna suala la kununua vitendea kazi kila tulikopita Halmashauri zinalalamika hazina vitendea kazi, havina magari unakwendaje kupima kule huwezi kumfikisha yule mtaalam kwenye eneo. Kwa hiyo, kuna vitendea kazi ikiwemo pamoja na magari kwa ajili ya kufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo bado kuna ku- support Mabaraza, tumesema Mabaraza hayafanyi kazi vizuri, mradi huu unakwenda kuboresha Mabaraza kuweza kuyapa vitendea kazi, waweze kuboresha kazi zao na Mabaraza ambayo yanazungumzwa kwamba hayajafika katika Wilaya zote, Mabaraza yamefika Wilaya zote 139 kwa maana ya kuundwa, lakini katika utendaji wake ni Mabaraza 88 ambayo ndiyo yana Wenyeviti wa Mabaraza, lakini hakuna ambalo alihudumiwi kwa sababu unakuta Mwenyekiti mmoja anahudumia labda Wilaya mbili. Ukichukua kwa mfano hapa Dodoma tunao Wenyeviti wawili, mmoja anahudumia pia Kongwa na Bahi mwingine anahudumia Mpwapwa ahaa sorry Mpwapwa na Kongwa, huyu mwingine anahudumia hapa Bahi, Kondoa ndiyo linajitegemea.

Mheshimiwa Mwneyekiti, kwa maana hiyo nikwamba kote wanafikiwa, lakini cha msingi tu nikwamba tuna upungufu wa hao Wenyeviti ambao tayari kuna Wenyeviti 34 ambao wanahamia kutoka kwenye Idara tuliomba hapa, tuliomba katika Wizara kwamba wale ambao ni wanataaluma waweze kuja kwa ajili ya ku- support, tayari 34 wamepatikana, kwa hiyo wakija katika ile 55 ambao ina upungufu tutakuwa pia tumepunguza gap na vilevile Bunge hili lilishauri kwamba hawa wanapokuwa na mkataba kazi haziendi vizuri. Sasa hivi walishakubaliwa kuwa waajiriwa, maana yake ni kwamba fursa za kuajiri zikitoka tutakuwa tumeziba gap tena hawa wanaohamia na hawa wengine tutakuwa tayari tumewapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo yale yote ambayo yanaelekezwa na Kamati tunayatekeleza japokuwa yanakwenda hatua kwa hatua kwa sababu huwezi kwenda ukayamaliza yote kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa suala la kodi kwenye masuala mazima ya makampuni kutolipa na mimi nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa nchi hii Dkt. Samia Suluhu Hassan alitoa msamaha kwa watu kulipa kodi bila riba na katika hayo baadhi ya makampuni yameweza kuitikia kati ya makampuni hayo tunayo VETA, tunayo TTCL, tunayo PSSSF, tunayo VETA hizi ni taasisi za Serikali, zimeitikia na kuweza kufaidika katika huo msamaha, lakini bado kama Serikali kuna utaratibu ambao umewekwa kuhakikisha kwamba taasisi zote za umma zinalipa kodi, kwa sababu kodi hiyo hiyo ndiyo inakwenda ku-supplement kwenye matumizi ya Serikali kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunachofanya hapa ni kuhakikisha kila hatua inayoelekezwa tunaifanyia kazi, kila hatua, hakuna hata moja ambalo tumeliacha. Kwa hiyo, ninachotaka kusema katika hili, kila ambacho kimetolewa maelekezo tunayafanyia kazi kulingana na maelekezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu huu mradi pia umekuwa na kelele nitakukabidhi karatasi hii ambayo inaonesha kila item itakavyokwenda kufanyiwa kazi na pesa yake iliyopangwa. Kwa hiyo, ukiipata hii ndio utajua. Maana unapo-combine bila kujua kila kipengele kinafanya kazi gani, huwezi kupata picha halisi. Nitaomba nikukabidhi hii ili pia iweze kukuongoza kuhusu kile ambacho Waheshimiwa Wabunge wanakilalamikia na kile ambacho kimepangwa kwenye mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala ambayo yamezungumzwa mengine pia kuhusiana na Sera ya Ardhi ya Mwaka 1995 ambayo rasimu yake ilikwishakamilika toka Julai, 2021. Sera hii bado haijatoka kulingana na mabadiliko ambayo tunakuwa nayo kwa sababu, tulikuwa tunahitaji pia kuwa na sera ya nyumba, lakini pia tunahitaji kuwa na sera ya makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hizo sera kuna mahali ambapo zinaingiliana kutokana na mabadiliko yanavyokuja. Unapokaribisha na wawekezaji na nini, unakuta sera haziwabebi kulingana na jinsi ambavyo matakwa ya nchi yanataka. Kwa hiyo, katika hili tunaendelea na rasimu ambayo inaandaliwa, baadaye tuweze kuja ku-harmonize na wenzetu. Kwa mfano wenzetu wa Mambo ya Nje wanatengeneza Sera ya Diaspora ambayo sasa nao watahitaji masuala ya kuwekeza na kuweza kumiliki wakati mwingine. Sasa hii bila kuwa na sera huwezi kupata, kwa hiyo, lazima tukamilishe hii halafu twende kwenye sheria. Kwa hiyo, haya yote tunayaweka katika ule utaratibu ambao umekubalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chege alizungumzia suala la miradi kutokukamilika. Katika ile miradi ya NHC, tuishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, wameridhia sasa NHC kukopa pesa na wameshakubaliwa kukopa bilioni 173 ambazo zitakwenda kukamilisha hii miradi ambayo ilikuwa imesimama kwa muda mrefu. Tunachofanya ni mambo mawili; kuna hiyo pesa ya kukopa, lakini kuna hii pesa ambayo imetajwa ya bilioni 47 ambazo ni accrued interest katika mradi ule kusimama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya tutafanya mazungumzo na yule mkandarsi ili kuona tunatokaje katika hili kwa sababu, kama pesa imepatikana maana yake ujenzi utaendelea. Kwa hiyo, masuala ya accrued interest ambayo anatudai basi tunaweza kuona ni jinsi gani tunaweza tukaongea nao na tukaweza kumaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika haya masuala ambayo yote yamezungumzwa nilitaka nitolee ufafanuzi huo kwa sababu ni mambo ambayo yanahitaji pia kwenda kwa pamoja katika uelewa. Nirekebishe pia, taarifa ya Mheshimiwa Hawa aliposema kwamba, huu mradi haujui ndio ameusikia hapa. Mradi huu ulianza kuandaliwa 2016, tukaanza discussion 2018, mwaka 2021 mradi ukakubalika, mwaka 2022 ukasainiwa na bajeti ya mwaka jana kwenye hotuba ya Waziri na pamoja kwenye randama mradi huu upo na Mbunge alikuwa ni Mjumbe wa Kamati na wala hajabadilishwa yupo. Sasa anaposema anakuja kuusikia hapa, basi niombe tu wakati mwingine tunapotoa taarifa, basi Wajumbe wawe wanazipitia vizuri kuliko kuja kutoa taarifa ambazo sio sahihi katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Nianze kwanza kwa kuishukuru sana Kamati na kuunga mkono pengine na kusema kwamba tunapokea ushauri ambao wameutoa ikiwa ni pamoja na ile addendum ambayo imeletwa kama Serikali tumeipokea na tutakwenda kuifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji wengi wamezungumzia masuala ya migogoro na kama mwenzangu wa kilimo alivyozungumza, suala hili la migogoro ni mtambuka. Nitapitia wachache ambao nimejaribu ku-note, ukiangalia suala la migogoro, zaidi ya Wabunge 15 wamezungumzia. Naomba nianze kwa kusema kwamba ushauri uliotolewa na Kamati tumeupokea kama ulivyo, wamezungumzia suala la National Housing kwamba nyumba ni za gharama nafuu, lakini ubora si mzuri sana. Hilo tumelipokea na tutakwenda kupitia tena kuona ni jinsi gani ambavyo watakwenda kuboresha. Sehemu kubwa pia hata ile size ya nyumba zinapoungwa mbili wengi wamesema hawazipendi sana katika kutembelea waliyazungumza hayo. Kwa hiyo, tutalifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikija kwa hoja ya Mheshimiwa Sakaya ambayo alizungumzia habari ya Kamati iliyoundwa na Wizara tano ambazo hazijajulikana zinamaliza muda wake lini pamoja na Mheshimiwa Grace Kiwelu na Mheshimiwa Pauline Gekul wote walitaka kujua taarifa hizi zitakuja lini.
Mimi niseme tu kwamba tarehe 13 Februari, taarifa ya kwanza itatoka na wamepitia katika mikoa mitano, wamekwenda Tabora, Katavi, Morogoro, Geita na Kagera. Kwa hiyo, taarifa ya kwanza tutaipokea kutoka katika mikoa hiyo. Baada ya hapo awamu ya pili wanakwenda katika Mkoa wa Arusha, Manyara, Tanga na Pwani, kwa hiyo, tutawapa ratiba kamili watakapokuwa wanakwenda kule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Sakaya pia alitaka kujua namna ambavyo tunaweza tukasaidia Halmashauri kuhakikisha kwamba viwanja vinapimwa na kuondoa hii migogoro. Niseme tulikuwa na ule mfuko na bado upo lakini haufanyi kazi vizuri sana kwa sababu Halmashauri zetu zinakopa na hazirudishi. Jumla ya Halmashauri 27 zilishakopeshwa kiasi cha shilingi 962,676,000 lakini kati ya hizo Halmashauri 11 hazijalipa, bado zinadaiwa. Kwa hiyo, pesa ambayo ilitakiwa irudi ni shilingi 1,155,211,224.
Kwa hiyo, niwaombe tu Halmashauri ambazo zinadaiwa mrejeshe ikiwemo Halmashauri ya Magu, Mji Mdogo wa Makambako, Kagera, Bunda kwa maana ya Chato lakini kuna Singida, Sengerema, Iringa, Tumalenga, Ruvuma, Songea na Tarime. Hizi ni Halmashauri zinazodaiwa, tuwaombe sana mrejeshe ile mikopo ili na wengine waweze kutumia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa suala la kusaidia, tuseme tu kwamba kanda zetu tumejaribu kuziimarisha, lakini tatizo tulilonalo kwa nchi nzima tuna upungufu wa watumishi wa sekta ya ardhi kwa asilimia 64. Kwa hiyo, utaona kwamba kuna upungufu mkubwa ambapo kwa kweli kuweza kukidhi haja inakuwa ni ngumu. Pamoja na upungufu huo, tunazo Halmashauri kama saba ambazo hazina kabisa wataalam hao, kwa hiyo, unaweza ukaona changamoto jinsi ilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ambavyo tunajaribu kuimarisha kanda zetu, niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge pale mnapokuwa na ratiba za upimaji shirikisheni ofisi zetu za kanda, kwa sababu tunatarajia watakuwa tayari wamekamilika na timu nzima za wataalam lakini pia na vifaa vya upimaji. Kwa sababu unakuta kanda moja pengine inasimamia Halmashauri zaidi ya 18 mpaka 36, basi niombe tu ile ratiba iweze kwenda vizuri ili hawa nao wasaidie katika kupima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sehemu kubwa ni jukumu letu katika Halmashauri zetu kuona ni jinsi gani tunapanga mikakati yetu vizuri kuweza kuweka utaratibu wa kupima kila mwaka na kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi, tukiweka angalau vijiji vitatuau vinne kila mwaka tutasogea. Gharama siyo kubwa ni kati ya shilingi milioni sita mpaka 7 na kuna vijiji vingine vina uwezo basi tuwashirikishe wale waweze kuona ni jinsi gani wanaweza wakahudumiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ku-subsidized nyumba za National Housing hili tulichukue tu tulifanyie kazi, kwa sababu ni mashirika mengi yanayojenga, bado TBA, WatumishiHousing, NSSF kila mmoja atataka kunufaika na punguzo hilo. Kwa hiyo, niombe tulichukue tutaendelea kulifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la mashamba ambapo wamezungumzia kwamba kasi ni ndogo pengine na gharama ya kuweza kuyapima. Mimi niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwenye maeneo yetu sisi ndiyo tuna mashamba hayo na tunatambua jinsi gani ambavyo hayajaendelezwa. Kazi ya Wizara ni kupokea kile ambacho mmeona hakifanyi kazi vizuri na kimekiuka taratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuwaombe wakati wanafanya kazi zao wale watumishi wa idara husika iwe ni sehemu ya kazi zao. Mmaana hapa mmesema hakuna pesa anahitaji pesa lakini akiweka kama ni sehemu ya kazi zake za kila siku, yule anayefanya kazi za uandani anapokwenda kufanya kazi kule basi afanye na kazi hii itasaidia sana katika kuona ni jinsi gani tunaweza tukapunguza au tukatoa taarifa za haya mashamba. Tusisubiri hela za kuja kupimiwa au kukaguliwa kutoka Wizarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Njeza amezungumzia suala la mipango miji, naomba nikiri tu hili nalo ni kutokana na upungufu tulionao. Pia tunaomba sana kwa sababu wenzetu wa Mbeya wako katika mpango kabambe wa master plan basi hilo nalo liingie katika mpango huo, itasaidia sana katika kuona ni jinsi gani tunaweza tukaweka mpango mzuri katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la ile project ya Kawe, imezunguziwa kwamba amepewa mtu binafsi kwa US dollar milioni 6.5.
Naomba niseme tu kwamba tungeweza hata kuishukuru Serikali kwa namna ilivyoweza kuokoa, kwa sababu lile lilikuwa imewekwa chini ya PSRC na ndipo hapo Wizara ikaomba kupitia National Housing ili kuweza kuchukua ile fifty, fifty angalau eneo lingine lirudi Serikalini. Isingekuwa hivyo basi basi eneo lote lilikuwa limeshaondoka. Mimi nasema kwa kweli lile eneo na gharama yake ni kubwa kwa maana ya kwamba lina-appreciate kila siku. Kwa hiyo, kitendo cha kuchukua asilimia 50 ...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ametujalia uhai mpaka tumefika hatua hii tunapokwenda kuhitimisha hoja ya bajeti ya Wizara ya Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee kabisa niwapongeze na kuwashukuru Wabunge wote ambao kwa namna walivyochangia Wizara hii ya Ardhi. Wengi wamechangia kwa uchungu sana na wamechangia wakiwa na imani ya kwamba kile wanachokizungumza kikifanyiwa kazi maana yake Watanzania wengi wataweza kuwa na amani. Nina washukuru sana kwa sababu ni dhamira njema ya Serikali kuhakikisha kwamba watu wao wanaishi kwa amani na hili sisi kama Wizara tumelichukua, tunaona ni jambo la msingi na michango yote iliyotolewa yote ilikuwa ni michango ya busara ambayo inahitaji kuifanyia kazi kwa namna moja ama nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nishukuru pongezi mlizozitoa kwa Wizara na Serikali hasa kwa Mheshimiwa Rais. Kwa kweli kama ni pongezi zote mlizozitoa kwa Mheshimiwa Rais ni hakika zinamstahili, kwa sababu katika mageuzi makubwa yanayofanyika ndani ya Wizara kuna mkono asilimia 100 kutoka Mheshimiwa Rais. Wote mnajua Wizara ilikotoka na Wizara ilipo sasa kwa kwa uhakika Wizara ilipo sasa haianzishi migogoro mipya, bali inahangaika na migogoro ambayoo imekuwepo ya miaka nenda-rudi, lakini kwa miundombinu ambayo tunakwenda kuwekeza tuna imani tutakwenda kuimaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika uchangiaji jumla ya Wabunge 34 wamechangia 30 wakiwa wamechangia kwa kuwaongea na wanne wamechangia kwa maandishi, niombe kutolea ufafanuzi kwa hoja za Wabunge ambazo wamezitoa katika mjadala huu ambao ulikuwa unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na lile ambalo lilikuwa linaongelewa ya kwamba Serikali ilikosea sana kuwahamisha watumishi wa TAMISEMI na kuwapeleka Wizara ya Ardhi.

Naomba niseme tu kwamba sababu za msingi zilizopelekea Serikali kufanya jambo hilo ni kwamba sheria zote zinazohusu masuala ya ardhi zimekasimiwa mamlaka na usimamizi wa ardhi kutoka kwa Waziri mwenye dhamana. Sasa hawezi kuwa Waziri mwenye dhamana wakati wale ambao unawasimamia hawako kwako wewe siyo mamlaka ya nidhamu, wakifanya kosa la kiutalamu, wakifanya kosa la kiutumishi, huna mamlaka ya kuweza kuwagusa, lakini wanachokifanya ni kile ambacho wewe umepewa dhamana ya kusimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kitendo cha kuwahamisha kuwaleta katika Wizara, Serikali ilikuwa na lengo zuri la kutaka kuwaweka katika mstari ambao utaweza kusimamiwa kitaaluma, kwanza kutoka kwa Waziri mwenye dhamana mwenyewe, lakini pia katika usimamizi wao kuna bodi ambazo zinawasimamia na zote ziko chini ya Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia pia Sheria ya Ardhi Sura 113 kifungu cha 8 cha sheria hiyo na kifungu cha 5 cha Mipango Miji kwenye Sheria Namba Nane ya mwaka 2007 aya ya 18.11 na bahati nzuri mtoa hoja alikuwa ni mwanasheria anajua hii. Kwa hiyo, Serikali imeweka hiyo kuhakikisha ya kwamba haya yanakwenda katika utaratibu huo. Lakini pia majukumu ya Wizara wameainishwa kwenye Tamko la Mheshimiwa Rais Namba 385 la tarehe 7 Mei, 2021 na Waraka huu wa Utumishi Namba 01 wa mwaka 1998 ulifanyiwa marekebisho mwaka 2019 na katika kufanya hivyo sekta tatu zilitolewa kwa wakati mmoja; maji, barabara pamoja na ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Wizara ya Maji, niwapongeze pia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ambao tayari waliunda vitengo. Sasa ukiangalia namna bora ya utoaji huduma kwa maji ndiyo hiyo hiyo inatakiwa ikawe bora katika sekta ya ardhi ambayo ni Wizara wezeshi katika suala zima la kuweza kutoa huduma kwa wananchi.

Kwa hiyo, katika hiki ambacho tunakifanya sisi sasa ni kwamba watumishi wameletwa Wizarani waweze kusimamiwa na hatua mbalimbali zimechukuliwa katika wale ambao wamesababisha migogoro ikiwepo hapa Mkoa wa Dodoma watumishi wengi wameachishwa kazi na wengine wamepewa maonyo kwa sababu tu ya kukiuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama huyo mtu hauko nae ndani ya Wizara yako anayefanya sekta yako huwezi kumsimamia, lakini hatua hiyo pia ilikuwa imelenga suala zima la kuboresha na tunavyokwenda hata mabadiliko ambayo Mheshimiwa Hawa Mwaifunga ameyasema, yanafanyika kwa nia njema na dhamira njema ya kuwasikiliza Waheshimiwa Wabunge analalamikia labda mtu huyu hafanyi kazi vizuri, unachunguza unakuta labda kazi haiendi vizuri, lakini wakati mwingine anafanya vizuri katika kuboresha zaidi unamtoa pale alipo, unapeleka kwenye changamoto nyingi ili aweze kuzitatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano yule wa Tabora ametoka Tabora ameletwa Dodoma na anafanya kazi nzuri sana. Aliyekuwepo Dodoma hapa naye amepanda cheo kafika hatua ya kwenye nafasi nyingine nzuri zaidi. Kwa hiyo, ni kwamba tunapeleka huduma hii kulingana na uhitaji uliopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo nitamuomba tu aliyetoa hoja hiyo atuletee watumishi au Halmashauri zilizogoma kufanya kazi kwa sababu tu zimehamishiwa Wizara ya Ardhi. Sisi kama Wizara hatuna taarifa wala nyaraka zozote za watumishi kuamua kuacha kazi au kugomea kazi, kwa sababu tu wametoka katika Wizara ya TAMISEMI na kupelekwa Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaomba sana hilo tulipate kwa maandishi ili tuweze kufuatilia hao na tujue kwa nini wametoka maana hatuna taarifa hiyo tumeisikia hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala lingine ambalo amelizungumza Mheshimiwa Mtemvu; mimi nimpongeze sana Mheshimiwa Mtemvu amekuwa akiliongelea sana suala hili la maeneo ambayo yamechakaa na kutaka pengine kufanya miji yetu ipendeze. Niseme kwa Watanzania hii ni fursa ambayo hata yule Mtanzania wa kawaida mwenye ardhi yake mjini ambaye ana nyumba yake ya toka mwaka 1947 lakini unapoangalia mipango ya majiji yetu na miji yetu pale alipo sasa hapatakiwi kuwa na jengo kama lile. Niwaombe sana wasiuze maeneo na kuondoka, lakini watumie ardhi zao kuwezesha kujinufaisha na kuleta utajiri, waingie kwenye ubia kama una jenga ghorofa tano pale mwenye hati ni mimi nina jengo langu la kawaida wewe jenga ghorofa zako tano tukubaliane zangu ni ngapi? Maisha yanaendelea mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kumejitokeza wahuni wachache wanaenda katika maeneo hayo hasa kwa akinamama waliozeeka zaidi wanawadanganya, wanawanyang’anya zile ardhi na mtu anajenga jumba pale anaendelea na kufaidika, lakini yule aliyoitunza ile ardhi kwa muda mrefu anakosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Jiji la Dar es salaam kumekuwa na mipango mingi zaidi ya kumi ambayo imefanyika tulikuwa na Buguruni Development Plan ya 2014-2024 inakwenda kuisha na hali inayokwenda katika uendelezaji bado ni wa kusuasua. Kuna Kurasini Development, kuna Dar es salaam Central Area Development Scheme ya 2018 – 2028; kuna Magomeni ambayo imeshaanza sasa hivi ile Magomeni Quarter tunaona inavyokwenda na ndiyo muelekeo. Kwa hiyo, plan ziko nyingi kinachotakiwa ni zile Mamlaka za Usimamizi za Upangaji kuweza kutekeleza hiyo mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wakati mwingine tunachanganya, sisi kama Wizara tunasimamia sera, kanuni na miongozo mbalimbali suala la uendelezaji miji lina mamlaka yake ya kusimamia, lakini kwa sababu Serikali ni moja na tunafanya kazi moja, ukiona mambo hayaendi vizuri unatia mkono katika kuhakikisha kwamba suala hili linakwenda vizuri.

Kwa hiyo, katika mambo ya ushauri mliyoyatoa tunayachukua na nimshukuru sana Mheshimiwa Angellah Kairuki anayesimamia mamlaka za upangaji, amejibu suala la migogoro na mambo mengine ambayo pengine mamlaka za upangaji zinatakiwa kuisimamia kwa karibu hasa walioko kule chini Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mtemvu ameenda mbali zaidi akasema tuangalie namna bora ya kuendeleza maeneo ambayo pengine yamechakaa kwa kutumia National Housing. Mpaka sasa National Housing kazi inayofanyika ni nzuri na katika ufanyaji kazi wake tayari wameishaingia katika mikataba mbalimbali wakati wa hotuba yangu nilizungumza na hiyo haiishii katika wafanyabiashara tu, inakwenda pia katika kubadilisha kabisa maeneo mengine ambayo yapo na tayari katika mipango yao wamefungua milango ili watu waweze kuingia, na Mheshimiwa Rais kafungua milango kuruhusu wawekezaji kutoka nje na ndani ya nchi wachukue fursa hiyo sasa kwa sababu suala la uendelezaji milki bado liko chini sana tunahitaji kuongeza kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, milango imefunguliwa kwa hiyo anatakiwa kuingia kusaidiana na Shirika la Nyumba, lakini bado anaweza akaingia na mtu binafsi kama nilivyosema, lakini bado hata kama wewe Mheshimiwa Mbunge una ardhi yako bado ni ruksa kuingia katika makubaliano na likaendelezwa tukabdilisha sura ya miji yetu. Magomeni Quarter ni mfano mzuri na tumekwenda kujifunza hata kwa wenzetu Morocco walikuwa wanakweneda block kwa block wanaondoa zile squatters wanajenga majengo, lakini wale walioko pale hawaondolewi, wanatolewa kwa muda wanakaa sehemu baadaye majengo yakikamilika wanaingia na maisha yanakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Halima Mdee amezungumzia habari ya National Housing katika mradi ule wa Kawe Seven Eleven pamoja na ile miradi mingine ambayo ameitaja. Naomba tu niseme ya kwamba ni kweli NHC kuna kipindi walisimamishwa kuchukua mikopo wasiendeleze maeneo yao na wakati wanasimamishwa kulikuwa na miradi mikubwa inaendelea pamoja na Mororcco Square ambayo sasa imekamilika. Kwa hiyo, Serikali kwa kushirikiana na Shirika lenyewe la Nyumba katika suala zima la kuondokana na hili suala Mheshimiwa Rais ameridhia National Housing waendelee kukopa na wameshakopeshwa, wamekubaliwa kukopa shilingi bilioni 173 ambazo sasa zinakwenda kukamilisha ile na hao ambao miradi yao ilikuwa imesimama ambao pengine wangeweza kuidai National Housing, tayari tuko nao katika mazungumzo kuweza kuona ni kwa namna gani pengine ubia uliokuwa unaendelea katika kufanya kazi au ule ukandarasi uliokuwa unaendelea utaendelea bila kuingiaza hasara National Housing kwa sababu kosa lile halikuwa la National Housing na ndio maana Serikali imeingia kwa karibu sana kuweza kulizungumza suala hili liweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la migogoro ambayo imezungumzwa na Mheshimiwa Mwita Waitara, Mheshimiwa Bahati, Mheshimiwa Halima Mdee, Mheshimiwa Ester Bulaya, Mheshimiwa Yahaya, Mheshimiwa Ally Makoa na Mheshimiwa Robert nadhani Wabunge kama kumi hivi wamezungumzia suala la migogoro hasa ya vijiji 975. Nimshukuru sana Mheshimiwa Mary Masanja ameweza kujibu kwa namna nyingne ambayo imekwenda kulizungumzia hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme tu, migogoro hii kama tulivyosema ni ya muda mrefu, lakini imekuwa sugu kwa sababu kule chini ambako ndio mgogoro unaanzia, wanaacha mgogoro unaanza mpaka unafukuta unafikia mahali ambako hauwezi tena kusuluhishwa. Lakini kama tungekuwa tunafanya kazi kule, bahati nzuri sisi wote ni Madiwani na migogoro yote hii iko kwenye maeneo yetu, tunasikia mpaka hapa na hapa kuna kelele, lakini tumekaa kimya tunasubiri kuyaleta kwenye Bunge. Tukiyasimamia kule kule chini hasa wale watendaji wetu, kwa sababu ndio jukumu lao, kama GN imezungumza habari ya maeneo ya utawala na kazi ya Wizara ya Ardhi ni kutafsiri GN, kazi yake ni kutafsiri GN ambayo mipaka inakuwa imewekwa inaweza ikawekwa kwa features zilizoko ardhini au kwa kufata coordinates na katika maeneo ambayo tunafata coordinates peke yake wananchi wengi wanakataa, lakini ukienda kwenye milima ukienda kwenye mito, mito inahama leo ulikuwa umeweka coordinates kesho inakataa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo matokeo yake ni kwamba tunakwenda na vyote viwili kunakuwa na coordinates lakini na zile features zilizoko ardhini. Lakini sasa wananchi wetu mara nyingi wengi hawataki kukubali ule ukweli hata wale walioingia katika maeneo hawataki kukubali ukweli na sheria haiwezi kusema uongo katika masuala ya tafsiri. Bahati nzuri ukienda kwenye migogoro wanakwambia tafsiri iliyoko kwenye GN au GN iliyoko wanaitambua. Ukisema unaenda kufanya tafsiri kwenye ardhi anakataa, sasa tunataka kujiuliza katika hilo kipi ambacho unakiona kinafaa? Ukienda kwenye ramani iko sawa, lakini mwananchi anasema hapana sisi hapa kulikuwa na mto, lakini mto haupo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa lazima tufate taratibu zile zote za kitaalamu na haya yameweza kupelekea Mheshimiwa Rais aridhie kwa sababu ya wananchi ambao walikuwa wamekaa maeneo mengi, ameweza kuridhia ekari 2,385,316 kuwapa wananchi pamoja na kwamba waliingia katika maeneo ambayo hayapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais katika hili kwa sababu amepunguza migogoro na kero za wananchi. Niwaombe tu Watanzania wenzangu pale ambapo Mheshimiwa Rais amesharidhia, mipaka tumeshaibadilisha, tumeshaweka mipya na tumeshaweka zile alama kwa maana ya beacon tuheshimu, kwa sababu changamoto nyingine zinakuja mpaka umewekwa na unaonekana, lakini mtu anavuka anaingia kule ndani. Ukienda kule unaingia kijinai, maana yake wewe ni mhalifu kama wahalifu wengine. Lakini tukisema siku zote tusitekeleze kile ambacho kiko kisheria inaweza ikatuletea shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ya migogoro ambayo ipo mimi nitoe rai tu kwa Watanzania wenzangu wote tutii sheria bila shuruti kwa sababu ardhi ndio wezeshi katika shughuli zote za kimaendeleo, ukiwa na mgogoro huwezi kwenda popote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Nyatwali na fidia; bahati nzuri alilianzisha Mheshimiwa Halima akalizungumza, akaja Mheshimiwa Ester mtoto wa pale pale akalizungumza, akaja na Mheshimiwa Getere naye akalizungumza. Wamelizungumza kwa uchungu sana na sisi tunakubaliana na hisia wanayokuwa nayo, lakini Serikali inachokifanya haina maana yoyote, yaani haina lengo la kudhulumu mwananchi yoyote. Katika masuala mazima ambayo yamefanyika hakuna mwananchi aliyedhulumiwa. Kabla ya kufanya uthamini kuna utafiti unafanyika, bahati nzuri wanasheria wanajua wanazisoma sana hizi sheria, kile ambacho wananchi walikuwa wanauziana na kile ambacho Serikali inatoa ni vitu viwili tofauti. Serikali imetoa kikubwa kuliko kile walichokuwa wanauziana, kwa hiyo, kinachofanyika pale wananchi tunayo na mikataba yao walikuwa wanauziana wengine ekari moja shilingi 500,000 wameenda sana mpaka shilingi 1,500,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ikaongeza pale top-up pale ya shilingi 500,000 lakini thamani ya ardhi ya pale haifiki ile thamani ambayo wamepewa. Kwa hiyo, mimi niseme tu kwamba Serikali haina dhamira ya kumnyanyasa Mtanzania lakini Serikali ina dhamira ya dhati kuhakikisha kwamba inalinda pia maisha ya Mtanzania katika kuwezesha kuweza kumlipa pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bahati amezungumza kwa kirefu sana amesema nisipotaja maeneo ambayo yametolewa kwa sababu amekuwa akisikia Waziri Mkuu kasema hivi, statement ya Waziri Mkuu na tunayosema Wizara ni ile ile wala haina tofauti yoyote. Katika eneo la Hifadhi ya Ruaha kule Mbarali jumla ya vijiji 13 vimeondolewa katika maeneo ya hifadhi ambavyo ulitaka tuvitaje ni Azimio, Igava, Ruiwa - Mahango, Mapogoro, Mbalino, Miyombweni, Mlungu, mpolo, Mwatenga, Nyakazobe, Magululu, Sonyanga na majina magumu kweli kweli, lakini ndiyo hivyo tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji ambavyo vyote vimebaki I mean vinatakiwa kutoka kwa 100% kwa maana ya vijiji ni Kijiji cha Msanga, Iyala, Makulusi, Kilambo na Luhanga. Lakini katika hivi vijiji vitongoji katika haya maeneo vitongoji 38 katika vijiji 16 vya Mwanavala, Imalilosongwe, Warumba, Igulunya, Vikai, Ikunda, Ihuta, Iwalanje, Magigiwa, Mkuya, Mahango, Nyamakuyu, Ukwavila, Mvunguni, Isimike na Ruanze vitaondolewa kupisha shughuli za hifadhi. Kati ya 38 kuna hivyo ambavyo vinaondoka.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu alichosema, alisema kwa idadi ya vijiji lakini kuna vijiji ambavyo sehemu yake ya vitongoji vinaondoka kwa maana ya kwamba havijaathiriwa na hifadhi na sehemu ambayo inaingia kwenye hifadhi yenyewe itabidi waondolewe. Kwa hiyo, vimewekwa kwa maana vijiji ni vitano, lakini vingine ni sehemu ya vitongoji ambayo vinabaki kwenye hifadhi. Pori la Swagaswaga ameshalizungumzia sitaki kulirudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye eneo ambalo limeleta changamoto kubwa kwa Wabunge wote wamelizungumza.

Kwanza naomba nikiri wazi tu kwamba mradi huu siyo mradi wa leo, mradi ulianza mwaka 2016 kwa maana ya kuanza mchakato. Mwaka 2018 ndio discussion zikaanza na wenzetu wa World Bank, mwaka 2021 wakakubali ku–finance na mradi huu uli–appear kwenye bajeti ya mwaka 2020/2021, ume–appear kwenye Bajeti ya 2021/2022 na sasa 2022/2023 ndio tumeanza kuutekeleza. Lakini mradi huo wakati wa makubaliano ulivyokuwa vijiji vilikuwa vimepangwa vilikuwa ni 250.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wa Kamati ninawashukuru walipiga kelele sana katika hili wakasema haiwezekani mnapeleka kwenye miundombinu pesa nyingi na nini tunataka vijiji viongezwe. Wizara ikaenda ikakaa, tukafanya mawasiliano na wenzetu ratiba zao kidogo zikawa haziko sawa sawa kwa sababu huwezi kufanya mabadiliko katika mkataba ambao mmeingia na World Bank bila kukaa nao na kuridhia. Lakini tuliangalia ndani ya mkataba ulivyokuwa na kwa sababu tulikuwa na ule mradi wa kuimarisha suala la upimaji kulikuwa na pesa ilikuwa imetengwa kwa ajili ya kununua ramani. Sasa mradi huu kama unafanya maana yake huhitaji kununua ramani, unaweza ukatengeneza mwenyewe. Tukahamisha zile pesa tukaenda kuongeza vikawa vijiji 250 suala ambalo tulitoa taarifa na walikubali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Waheshimiwa Wabunge naomba niwaambie, tumekaa miaka yote ya uhuru ambayo tunaizungumza vijiji 12,000 tunavyo 319 sasa ni 318 baada ya kijiji kimoja kuondoka. Lakini vijiji zaidi ya 10,000 vimepimwa na vina vyeti; vyenye mpango wa matumizi ni 2,675 kwa nini ni vichache? Kwa sababu hakuna miundombinu ya kurahisha upimaji na hiki kinachotakiwa kufanyika kinafanyika once and for all maana yake ni kwamba ukishasimika miundombinu ile ya upimaji, ukarahishisha ile distance ya upimaji kutoka kwenye kilometa 90 zikwa kilometa 20, 25 kasi ya kupima itaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika kuongeza kasi ya kupima hata ule uzalishaji wa viwanja, uzalishaji wa kupanga matumizi ya ardhi utakuwa mkubwa kwa sababu muda utakuwa ni mfupi na gharama itakuwa ni ndogo. Tukisema tuhamishe pesa tupeleke tukapime leo, bado kasi itakuwa ni ile ile ni ndogo utapeleka pesa lakini huna nyenzo za ku-speed up kazi yako. Bado utapima vijiji 50, utapima vijiji sijui vingapi kwa mwaka ambayo haifadhiliwi pia.

Kwa hiyo, kinachofanyika ndani ya Wizara ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na miundombinu ya uhakika ambayo haitaturudisha nyuma kwenye kasi, ukishaiweka maana yake sasa ni kazi ya kubanana kila mwaka hatuitaji kwenda kuweka miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo zile points ambazo zinatumika katika suala zima la upimaji ambazo zilikuwa tatu tu, sasa hivi tunaenda kuweka nyingine 30 na mradi unaweka 22 tunakwenda kuwa na kama 25 ambazo zile zinakurahishia katika kazi ya upimaji. Ukishaweka zile ndugu zangu kazi itakayobaki sasa kufanyika ni kazi ya kupima tu uwandani hata kama watafanya usiku na mchana, lakini wana uhakika na nyezo zile wanazozitumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili tutapeleka pesa ndio, lakini wana uwezo gani? Hawana vitendea kazi, zile mashine za kupimia za kileo, wanahangaika na total station, wanahangaika sijui na vitu gani, ambayo hayawezi kufanya kazi ile inayokusudiwa na lengo letu tupime vijiji vingi kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia pia tuna Dar es Salaam na Dodoma peke yake ambapo sasa tumewekea Mfumo wa ILMIS, tunakwenda kuweka Mfumo wa ILMIS kwa nchi nzima katika mikoa yote na ile inaweza kurahisisha sasa wale watendajii wanaokwenda kutumia hiyo mifumo hawana huo uelewa wa kuweza kuingia kwenye mfumo na kufanya kazi ile na ndio maana sasa hivi tuna timu ya wataalamu ambayo inahakikisha kwamba inaweka mfumo vizuri ina-clear data zote, halafu tunakwenda kusimika mifumo katika kila mikoa. Mifumo ile itatusaidia kuongeza kasi ya upimaji, kuongeza kasi ya upangaji, lakini kutunza kumbukumbu za kila mmiliki wa ardhi kiasi kwamba hatuwezi kuwa tena na kelele za double allocation, hatuwezi kuwa na kelele za upandanaji wa ramani hapa na pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la kufanya data conversion limefanyika kwa kiasi kikubwa 100% ramani za mipango miji pamoja na ile ambayo inakwenda kwenye ramani za upimaji wa ardhi, sasa usipokuwa na hiyo huwezi kwenda. Waheshimiwa Wabunge, tunaheshimu kile mnachokizungumza, wala hakuna ambaye hakiheshimu na ndio muelekeo tunaotaka sisi Watanzania wetu waweze kufikiwa, lakini tutaenda kwa kusuasua mpaka lini? Mimi nadhani hili mkiipa nafasi Serikali, halafu mkaja kuihoji hapa itakuwa ni vizuri zaidi, lakini ile dharura mnayoisema tunasahau kwamba hii ni fedha za kideni, kuna fluctuation ya currency na mpaka tunapoongea sasa hivi hizo dola mnazozisema hazipo, zimeshaliwa na mfumuko wa bei, kwa hiyo sio kwamba ni cash imewekwa ya dharura kwamba labda tutajisikia kama Wizara sasa tumepungukiwa tuchukue Hapana. Ile imewekwa kwa sababu kuu ya kuangalia mabadiliko ya currency zetu kwa maana ya inflation ambayo inakuwepo. Kwa hiyo, ni vitu ambavyo siyo kwamba tunaila sisi, na ukienda leo pesa imeingia toka mwaka jana jinsi ilivyokuja, ukienda sasa hivi siyo shilingi bilioni 345 tunazozisema leo, zimeshashuka kwa sababu siyo tena dola za Kimarekani milioni 150 kwa sababu ya suala la kibenki pia, kwa hiyo, ile siyo dharura ya kwamba inakwenda mfukoni kwa Waziri au kwa nani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika masuala haya niongelee suala zima la shamba lile la DDC la Mlolo Mheshimiwa Halima amesema. Mheshimiwa Halima wewe ni wakili, wewe ni wakili msomi na hili unalijua. Hivi kisheria unapokuwa na umiliki wa ardhi unaweza ukaukataa katika njia ipi? Una nyaraka ndio makaratasi sawa, lakini mwenye umiliki halali ana hati yake toka mwaka 1998 na bahati nzuri Mheshimiwa Gwajima leo hayuko hapa, wameshafanya vikao zaidi ya mara tatu wakishirikiana na wale DDC wenyewe pamoja na Mkuu wa Mkoa, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi wa Mkoa wa Dar es Salaam, walianzia shilingi 8,000 kwa square meter wananchi wakagoma, wakaja 6,000 wakagoma, wamekwenda kushuka kwa makubaliano wenyewe mpaka shilingi 4,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Halima unalolizungumza wale watu hawatalipa wasipimiwe ndio maana yake ile ardhi hawana faida nayo, hawawezi kuitumia mahala popote. Lengo la Serikali ni kuhakikisha wanamwezesha anapata hati na anakuwa mmiliki halali sio sasa leo unaambiwa ya DDC, kesho unatolewa na hayo hayo yako kule Chasimba Chachui.

Mheshimiwa Halima wananchi wamevamia maeneo lakini mtu tayari ana hukumu ya mahakama anatakiwa awaondoe, hasa katika kuwaondoa Serikali ime–intervene ikasema hebu tukae mezani, basi ninyi mmeshavamia hebu mrudishieni huyu hela yake ya ardhi aweze kuchukua ardhi nyingine na ninyi mmilikishwe muweze kutumia ardhi zile kisheria na kuweza kufanya kile ambacho kinaweza kuwasaidia katika maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuwaombe wananchi wetu kwanza wasivamie maeneo, kama wanataka kujenga wajenge maeneo kwa kufuata taratibu na kwa kutumia mamlaka za upangaji, asiingie kwenye eneo eti ni shamba limekuwa pori kwa muda mrefu halafu akasema kwamba hili sasa mwenyewe hayupo mimi naingia, tutakuwa tunafanya makosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu Mheshimiwa Kitandula namshukuru kwa hoja yake ambayo ilikuwa supported pia na Mwenyekiti wangu wa Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wizara tunapokea kile ambacho kimekuja kwa maana ya notice zinapokuja na kama zina kila ushahidi hamna tatizo. Sasa unapokuja shamba limepewa notice sawa muda umetosha anatakiwa kunyang’anywa, lakini hati yake iko kwenye benki. Sasa lazima taratibu nyingine za kifedha zifanyike, na huyu bahati mbaya zaidi amekopa benki ya nje na ndio maana kama mtakumbuka miaka mitatu iliyopita tulibadilisha sheria hapa kwamba ardhi ya Tanzania kama unataka kukopa ukope ndani ya nchi na ukaendeleze hapa hapa ndani ya nchi, kwa sababu tumekuta wengi walikuwa wamekopa zamani kwa kutumia mashamba hayo hayo na hawayaendelezi nawamekopa nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo pale tulikuwa tunaweka dhamana mbaya kwa Tanzania yetu kwamba ardhi yetu tunayo kubwa, lakini kwa sehemu tayari imeshawekwa dhamana nje ya nchi. Akishindwa kulipa huyo mtu anakuja na hati yake anadai ardhi yake, huwezi kukataa. Tukabdilisha sheria hapa nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge mlisaidia tulibadilisha sheria.

Kwa hiyo, mimi niwaombe tu Mheshimiwa Kitandula kwa sababu masuala mengine lazima yafate taratibu, tutalifuata tu kama ambavyo lilivyo na tutafikia maamuzi na Mheshimiwa Rais sasa hivi ukimplekea hati za kufuta wala haichukui muda, amefuta amshamba zaidi ya 11 Morogoro na wakarudishiwa wananchi pale kawa ajili ya kupanga matumizi mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hilo tunasema likishakamilika Mheshimiwa Rais hana neno na sisi kama Wizara, mimi kama mshauri nitapeleka kwa ajili ya kumshauri sasa afute ili ipangiwe matumizi mengine. Kwa hiyo, niwaombe tu kwamba maeneo yote hayo ambayo mnayazungumzia kwamba pengine mlishaomba yafutwe lakini hayajafanyika ni taratibu tu zikikamilka tunafuta. Changamoto tunayoipata tukiwarudishia kwenye Halmashauri/Mamlaka za Upangaji mnataka kupima viwanja vyote, mnasahau kwamba tunahitaji kuwa na mashamba. Kuna maeneo mengine hayatakiwi kuendelezwa I mean kurudishiwa ukapanga viwanja, bado lilikuwa ni shamba limeshindwa kuendelezwa na halijaharibiwa mle ndani kwa maana watu wameweka miundombinu ya kudumu labda majengo bado unaweza ukalitumia kama shamba na kwa mjini pia urban farming inakubalika heka tatu unalima. Sasa tutajikuta mjini kote tunajaza viwanja, viwanja halafu mashamba yanakosekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna mahali pengine pia tukiwaletea kwa ajili ya kufanya mpango wa matumizi basi tuombe tu tuangalie kama kweli tunatoka kwenye shamba tunaingia kwenye mji au tunafanyaje, lakini lengo la Serikali, lengo la Wizara ni kuhakikisha haya yote tunayafanya katika utaratibu ambao ni mzuri na haumuumizi mtu yeyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hoja ambazo zimezungumzwa zingine tutazileta kwa maandishi kwa sababu zilikuwa ni hoja nyingi, lakini nirudie kwa kusema tunaheshimu michango yenu na bahati nzuri katika lile suala la mradi Kamati ya Bajeti pia ilishalichukua na walikuwa wanalifanyia kazi. Kwa hiyo, tuna imani ya kwamba kile tulichiokieleza na kama kutakuwa na changamoto nyingine yoyote katika suala zima hili tutaweza kuona tunafanyaje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chege naye aliongea kwa uchungu sana suala la Utege, naomba tu nimwambie ya kwamba, sisi tutakuwa tayari kwa wakati wowote kuweza kuona ni jinsi gani tunaweza kutatua matatizo hayo bila kuwa na shida yoyote. Lengo letu ni kumsikiliza mwananchi aseme anachokisema na Serikali itaeleza kwa nini inataka kutwaa eneo lile, ili wote tuwe katika win-win situation kwa sababu, hakuna anayetaka kumuumiza mwenzie. Kwa hiyo, tukishamaliza hivyo maana yake mtu anapewa haki yake anayostahili na tunaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu ya kwamba kwa Wabunge wote changamoto zote mlizonazo tumezipokea. Kule tutakakotakiwa kufika tutafika, tutashirikiana na wenzetu wa mamlaka za upangaji kuhakikisha kwamba migogoro inatatuliwa. Hatuhitaji migogoro mipya, tunahitaji kumaliza iliyopo na kwa sababu tunaingia kwenye digitali, taarifa zote mtazipata kiganjani na haya ni mabadiliko makubwa chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Ardhi inakwenda kuwa Wizara wezeshi kikweli kweli na sio Wizara ya migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie katika Bajeti Kuu ya Serikali. Kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja kwa asilimia 100 bajeti ambayo imeletwa na Waziri wa Fedha; na nimpongeze sana pamoja na timu yake kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kiasi kwamba wamerahisisha mambo mengi kwa sababu imegusa maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuunga mkono niendelee kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo ameweka mkono wake kwa kiasi kikubwa sana katika bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wanachangia Waheshimiwa Wabunge kwenye bajeti wengi walikuwa wakilalamikia tozo mbalimbali ambazo zilikuwa pengine ni changamoto kwa wananchi na namna ambavyo wengi walikuwa wanakwepa kodi. Nakumbuka kuna baadhi ya Wabunge, Mheshimiwa Manyanya na Mheshimiwa Kamonga waliongelea habari ya capital gain. Capital gain mara nyingi watu wamekuwa wakinunua ardhi au wananunua nyumba kufanya transfer walikuwa wanakwepa kwa sababu ya kiwango kilikuwa kikubwa cha asilimia 10. Kwa kilio kile Mheshimiwa Rais amepunguza kutoka asilimia 10 mpaka asilimia 3 ni punguzo kubwa sana ambalo halijawahi kutokea. Mara nyingi tukipunguza tunakwenda kwenye 50 percent, lakini Mheshimiwa Rais amekwenda mbali zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe watanzania wale wote ambao walikuwa wanasita sasa kubadilisha hati zao kuwa kwenye majina yao wabadilishe kwa sababu tayari wameshapata fursa nzuri ya kuweza kumiliki ardhi zao kwa majina yao na wakatumia pia kwa shughuli za kimaendeleo. Punguzo hili limeleta nafuu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na hoja, walizungumza Mbunge alikuwa ananiuliza hapa kwamba na kwa wale warithi inakuwaje maana hawana uwezo. Naomba niseme kwenye suala la transfer kwa mrithi halipi ile capital gain tax kwa sababu ni transmission tu kutoka kwa mzazi kwenda kwa mrithi ambaye yupo kutoka kwa marehemu. Anacholipa yeye ni mambo ya stamp duty pamoja na ile gharama ya registration. Kwa hiyo nao pia watambue ya kwamba wana haki ya kuweza kumilikishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nimpongeze pia sana Mheshimiwa Rais na hasa katika suala zima la umiliki wa nyumba. Mara nyingi watu wengi wamekuwa wakiogopa, kwamba tunasema nyumba za gharama nafuu lakini bado walikuwa wanaona si gharama nafuu; na kubwa lililokuwa linaleta changamoto ilikuwa ni suala la VAT. Sasa Wizara ya Fedha wamekuja na pendekezo ambalo ni zuri kwa kushirikiana na wizara husika ambayo tunatarajia wale wote ambao walikuwa na mpango wa kumiliki nyumba hasa zile zinazouzwa na taasisi zetu National Housing, TBA, Watumishi Housing, NSSF, ambazo zinaitwa za gharama nafuu sasa watazinunua bila VAT. Kwa hiyo nasema tu kwamba tutumie fursa hiyo kwa sababu ni namna ambavyo unaweza kumwezesha mwananchi, akiweza kuipata ile pia ataitumia katika shughuli zingine za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii haikuishia hapo tu, wengi walikuwa wakilalamika gharama za umilikishaji zilikuwa ni kubwa kiasi kwamba wanashindwa kupima na kurasimisha maeneo yao; lakini sasa gharama za kumilikisha zimepunguzwa kwa asilimia 50. Maana yake ni kwamba yeyote yule ambaye alikuwa pengine ana hofu ya kuweza kuomba hati sasa hivi imepunguzwa. Tuna viwanja 1,500,000 ambavyo tayari umiliki wake, kwa maana ya kwamba vina watu lakini hawamiliki kisheria, na wote hawa walikuwa wanaogopa kwenye suala zima la tozo zile ambazo zinatakiwa kulipwa lakini sasa hivi malipo yote yamepunguzwa. Ukienda kwenye premium imepungua kutoka asilimia 0.5 imekwenda 0.25 iko kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, punguzo lingine la hati kutoka asilimia 20 kwenda asilimia 10, ile deed plan ambayo ilikuwa inachajiwa 20,000, tunaita kiziduo kwa lugha yetu ya Kiswahili, sasa hivi unaipata bure. Sasa hivi kila kitu kimeshuka na ile kiziduo tena hakichajiwi. Niwaombe sana Watanzania bajeti hii imeleta nafuu sana katika suala zima la umiliki wa ardhi pamoja na umiliki wa nyumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais aliona changamoto kubwa ya watanzania katika suala zima la ulipaji wa kodi alitoa nafuu. Haijawahi kutokea Mheshimiwa Rais yeyote yule katika historia ya Tanzania, aweze kutoa msamaha kwa miezi kumi haijawahi. Sana sana tutapata mwezi mmoja, miezi miwili maximum miezi mitatu. Lakini Mheshimiwa Rais alitoa msamaha huo kuanzia Julai, 2022 mpaka 31 Aprili na katika kipindi hicho watanzania waliochangamkia fursa wamejitokeza kwa wingi na tumeweza kukusanya bilioni 38 lakini tozo ambayo walisamehewa ni bilioni 27 na zile zilizosamehewa Watanzania hawa wanaweza kuzifanyia shughuli zingine. Kwa hiyo nachotaka kusema tu ni kwamba bajeti hii imegusa maisha ya mtanzania katika kila Nyanja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo suala zima la uwekezaji, wawekezaji wetu nchini wamekuwa pia wakitafuta ardhi ya kuwekeza lakini imechangiwa pia na Mheshimiwa Rais kufungua nchi. Katika kipindi kifupi hichi ambacho tumekuwa nacho tumetoa ardhi kwa wawekezaji yenye hekta 29,820 ambayo imeimngiza fedha za Kitanzania trilioni 7.8 na haya yote ni ule mtaji ambao wamewekeza. Kwa hiyo, kwa maana nyingine wanaporahisisha pia masharti mbalimbali katika suala zima la umiliki wa ardhi inaleta nafuu. Na hii imekwenda mbali zaidi sasa hivi, ukiangalia ile Sheria ya Uhamiaji namba 54 nayo pia kwenye habari ya resident permit imepunguzwa pia imewekwa kiasi cha dola 150. Mwenye mtaji wa dola 150,000 anaweza kujenga nyumba yake na anaweza akauza kama watanzania wengine na hii inafungua fursa pia kwa Diasporas ambao watatambuliwa kwa hati maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunasema bajeti hii inakwenda kugusa kila mmoja lakini inakwenda kukuza pia mtaji katika sekta ya nyumba ambako pia wawekezaji wamepewa fursa. Mara nyingi tulikuwa tunalalamika kwamba wawekezaji hawapewi fursa. Maana yake ni kwamba akijenga nyumba haondoki nayo, akikiuka masharti ya nchi manake ataondoka atatuachia nyumba yetu, hapo tayari atakuwa ameshaendeleza mji. Kwa hiyo hili nalo limeleta nafuu kubwa katika suala zima ambalo lilikuwa likipigiwa kelele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa kuliko yote katika suala zima la bajeti ya mwaka huu, ukilinganisha na bajeti ya mwaka jana; mwaka jana kwenye fedha zilizotengwa kwa ajili ya maendeleo zilikuwa ni bilioni 27 lakini mwaka huu fedha zilizotengwa kwa ajili ya maendeleo ni bilioni 82.13 sawa na ongezeko la asilimia 203 haijawahi kutokea. Ndiyo maana nasema Mheshimiwa Rais kwa kweli amefanya jambo la msingi sana na tukiangalia ardhi ndiyo sekta wezeshi katika maeneo mengine yote. Unapokuwa umewezeshwa katika suala zima la kuwa na program hii ya maendeleo ya sekta ya ardhi kwa kiasi kikubwa hiki tunachokipata ni utekelezaji wa kuzingatia sheria namna ambavyo Watanzania tunatakiwa tuzizingatie. Hii kwetu imekuwa ni rahisi kwa sababu tunakwenda kuwekeza pia katika miundombinu ya upimaji ambayo ilikuwa ina shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, mtakumbuka wakati mnachangia Wizara ya Ardhi mlipiga kelele sana kuhusiana na suala la kwenda kwenye vijiji, kwamba vijiji vilikuwa vichache. Kilio hicho kimesikika na kwenye bajeti kimeoneshwa ya kwamba sasa vijiji vitakavyokwenda kupimwa ni vijiji 2000 ambavyo vimeongezeka kutoka vile vijiji 250 vilivyokuwepo. Katika upimaji wa hivi vijiji pia vinatoka katika vijiji 1,059 ambavyo tayari vina mpango wa matumizi. Na katika suala hili kwa sababu tunahitaji pia kuona kwamba uwekezaji mkubwa unaenda kwenye sekta ya kilimo. Tumekuja kukubaliana na wenzetu wa kilimo kwamba, ardhi yote ya kilimo ambayo inafaa kwa kilimo itatambulika na itatangazwa katika gazeti la Serikali ili iweze kutunzwa kwa ajili ya uwekezaji kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wote ambao watapata fursa ya kupewa maeneo yale kwa ajili ya kilimo, niwaombe sana watimize masharti ambayo tunahitaji pengine kila mwekezaji anapopewa aweze kutumia eneo lake kwa faida na kama jinsi alivyoomba. Kuna wengi wanapewa ardhi lakini wanaiacha na watu wanavamia tunakuwa na migogoro. Naomba sana katika wale ambao watapata fursa ya kumilikishwa ardhi kipindi hiki niwaombe sana kwamba watekeleze masharti yote yanayotakikana ili tuweze kuondokana na kero ambayo tulikuwa nayo katika kipindi cha nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote yamefanyika katika sekta hii ya ardhi ambayo mara nyingi imekuwa na migogoro mingi lakini kwa hiki ambacho kimefanyika katika bajeti ya mwaka huu tuna imani tunakwenda kuboresha na hasa mifumo ambayo tayari tumekwishaanza. Sasa hivi ukiangalia hata usafishaji wa takwimu zetu, kwa maana ya data cleaning inaendelea kufanyika na nyingi zimefanyiwa tathmini na kuweza kurekebishwa, na tunakwenda kupata taarifa zetu kupitia kiganjani. Tulikuwa tunazungumzia habari ya maji unaweza kupata bili ukalipa sasa hivi pia kwenye sekta ya ardhi imekwishaanza na watu wameshaanza kupata taarifa zao kiganjani kama una deni unaletewa pale na unaweza kulipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo haya yote ni kwa sababu tu tumewezeshwa kama wizara kuhakikisha kwamba kila kitu kinakwenda sawa. Ninakushukuru nimekuibia dakika zako mbili lakini Mungu ni mwema nimemaliza niliotaka kusema, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Waheshimiwa Wabunge nianze kwa kumshukuru Mungu kwa fursa ambayo ametupa hadi tunafikia hatua hii tunapokwenda kuhitimisha hoja yetu. (Makofi)

Aidha, niungane pia na Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu kwa tuzo aliyoipata. Naomba niishie hapo kwa sababu pongezi nyingi zimetolewa lakini nia na dhamira ya dhati sana ni kwamba kuhakikisha watanzania kwamba tunaye Rais ambaye anafanya kazi na kazi hiyo inatambulika katika ulimwengu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge 27 waliochangia kwa kuzungumza na Wabunge wawili wamechangia kwa maandishi, kwa sababu hoja ni nyingi na nyingi zinahitaji maelezo ya msingi ili muweze kuzielewa vizuri tutaleta pia kitabu ambacho kitakuwa kinaelezea hoja moja baada ya nyingine. (Makofi)

Kwa hiyo kwa nafasi hii niliyopewa ya dakika 20 nitakwenda kujibu hoja chache ambazo zinahitaji maelezo ili tuweze kuona jinsi gani tunafahamisha kikao chako hiki cha Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja iliyopigiwa kelele sana na Waheshimiwa Wabunge hasa ile pia ya Mawaziri Wanane katika vile vijiji 975. Kama nilivyosema kwenye hotuba yangu tunastahili sana kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu vijiji vile 975 angekuwa ni Rais ambaye si msikivu asingeridhia vijiji 920 kuweza kuridhiwa na kurasimishwa na kupewa watu na tukumbuke katika changamoto hiyo ambayo ipo maeneo mengi ambayo yana migogoro kuna muingiliano wa matumizi ya ardhi unakuta kuna maeneo ambayo yalitengwa kwa ajili ya hifadhi lakini kutokana na sababu pengine ziwezi kusema zilisababishwa na nini tukajikuta tena tumeingia katika mgogoro mwingine wakuhalalisha vijiji ndani ya maeneo ambayo tayari yanahifadhi. Kwa hiyo, hapo ndipo mgogoro ulipoanzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika utatuzi maelekezo ndani ya Serikali ni kwamba lazima tuangalie vijiji ambavyo havina athari viweze kurasimishwa lakini tukumbe katika vijiji hivi 920 vinarasimishwa, vinavyobaki 55 shughuli inaendelea ya kufanyia tathimini. Tukumbuke katika hivi vijiji 55 tunayo miradi mikubwa ya kimkakati ambayo iko kwenye maeneo hayo, nikichukulia mfano wa Bwawa la Mwalimu Nyerere wote lazima tujiulize hivi lile bwawa kama halitaweza kupata maji ya kutosha na pesa yote iliyowekezwa pale maana yake Serikali itakuwa imepoteza fedha nyingi kwa ajili ya kutengeneza lile bwawa ambalo mwisho wa siku litakuwa halifanyi kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini maeneo yale yamezungukwa na watu ambao wanafanya kazi katika vyanzo vya maji ambavyo vinazuia maji kwenda katika ule mkondo ambao unapelekwa kwenye bwawa. Kwa hiyo, Serikali imejikita katika kufanya tathimini ya kina athari ambazo zinaweza kusababishwa na watu kuwepo na shughuli za kibinadamu na wakati huo huo bwawa linategemea maji yale. Kwa hiyo, kinachofanyika pamoja na Mawaziri Wanane kwenda kazi ya mikoa, lakini tukumbuke ile mikao saba au nane ya mwanzo Kamati ile inakwenda kwenye vijiji inaongea na wananchi na baadaye inakuja inawaachia mkoa kwendelea na hile shughuli na timu ya wataalamu inabaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukihesabu vijiji hivyo kama ngazi ya Taifa peke yake ndiyo itakuwa inakwenda kwenye maeneo, hiki tunachokipigia kelele cha migogoro itachelewa kutatuliwa kwa sababu siyo rahisi ngazi ya Taifa kwenda vijiji vyote na ukamaliza, tunaachia mamlaka ya mkoa, wanaofahamu maeneo yao, wanaoweza kuzungumza na watu pale na ambapo hata sisi tumeshatoa maelekezo.

Kwa hiyo tunachofanya kama Serikali ni kuwataka mamlaka zilizoko kwenye maeneo ambayo bado yanafanyiwa tathimini kuweza kuangalia uhalisia wakisaidiwa na wataalamu wetu, uhalisia wa maeneo yale yaachwe kama yalivyo, wananchi waendelee kufanya shughuli zao au kuna haja ya kuwaondoa wananchi maeneo yale ili miradi ile iwe salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hiyo tathimini yake bado inaendelea, kwa hiyo, mpaka sasa hapa ninapozungumza siwezi kukwambia nani na nani ataondoka pale ni mpaka ile tathimini ikamilike na wataalamu wapo. Na mimi niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, pesa nyingi mnahidhinisha kwa ajili ya miradi ya kitaifa, sasa tukiidhinisha pesa halafu sisi wenyewe tukataka kukwamisha mwisho wa siku tutakuwa tunapoteza nguvu ya umma lakini tutakuwa tunapoteza pesa ya Serikali kwa kukwamisha miradi ambayo tunajua kabisa ni vielelezo kwa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi niwaombe katika hivyo vijiji ambavyo tathimini inaendelea muwaamini viongozi wenu ndani ya mkoa, muwaamini viongozi wenu ndani ya Serikali hakuna utatuzi utakaokwenda kufanyika bila kushirikisha wananchi, wananchi watashirikishwa sehemu zote na maelekezo ya Serikali ndivyo yalivyo.

Kwa hiyo, tulikuwa tunakwenda kwa ajili ya kutoa maelekezo naomba sana hili lieleweke kwa sababu limechukua kidogo wazungumzaji wanaotoka katika maeneo hayo wamezungumza sana. Ikiwemo na GN 28 ambayo ni kati ya yale ambayo yanakwenda kufanyiwa kazi ukanda huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, limezungumzwa hapa suala la fidia, suala la fidia limekuwa ni changamoto na kizungumkuti katika maeneo mengi. Tunazo taasisi nyingi zinazodaiwa, Waheshimiwa Wabunge hapa wametaja baadhi, wametaja maeneo ambayo yamechukuliwa kwa muda mrefu na wengine wanasema karibu miaka 20, 25 lakini fidia hailipwi na tayari watu pale wanaathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke mwaka 2017 tulipitisha sheria hapa tukaipitia ile Sheria ya Fidia ambayo ilikuwa haina muda maalumu ambayo ilikuwa inaonesha kwamba watu wakitaka kutwaa eneo kama hajalipa fidia ndani ya muda kadhaa aweze kuendelea mwananchi na shughuli yake. Tulipitisha hapa kwamba ni ndani ya miaka miwili kama mlipa fidia hajalipa mwananchi anaendelea na shughuli yake, lakini hiyo ilikuwa yale maeneo ambayo yametwaliwa kwa sasa na kila baada ya miezi sita anakuwa charged na interest kama hatalipa.

Kwa hiyo, mimi niwatake mashirika yote na taasisi zote pamoja na wawekezaji ambao wanachukua maeneo ya wananchi kulipa fidia kwa wakati, vinginevyo Serikali haitakubali na hata kwenye hotuba yangu nimesema kama taasisi ya ushirika haijajiandaa katika kulipa fidia wasichukue maeneo ya watu, hilo ndiyo tunalolizungumza kwa sababu tunaleta kero ndani ya Serikali lakini unapotaka kufanya mradi lazima uwe umejiandaa kuhakikisha kwamba utalipa fidia hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo yaliyotajwa ya EPZA tayari Serikali imeshaanza kuyachukua baadhi ya maeneo ili mengine yanagaiwa wananchi, lakini pia nitoe tahadhari kule ambako maeneo yanarejeshwa tuweze kuweka mpango mzuri wa matumizi ili basi ardhi ili itufae katika matumizi. Kwa mfano maeneo ambayo yanakuwa yana mashamba, Wabunge wengi mmeomba mashamba wametaja Mbunge wa Mkinga kule ametaja na wengine wametaja kwamba kuna maeneo ambayo yapo tu yamekaa likiwepo shamba la Efatha limetajwa kwamba halijaendelezwa.

Naomba niseme ya kwamba maeneo ambayo yanaumiliki sahihi wa kisheria, taratibu zile za kuyatwaa lazima zizingatiwe. Kwa hiyo, inapofikia mwisho anayekwenda kubatilisha umiliki huo ni Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, ikienda kwa Mheshimiwa Rais na Waziri akimshauri Mheshimiwa Rais kubatilisha kama Mheshimiwa Rais akiona hii inafaa atafanya na kama alivyofanya na mpaka na kufuta yale mapori 12 ambayo wananchi wamepangiwa.

Kwa hiyo katika ufutaji au katika utwaaji lazima sheria zinafatwa. Kuna maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge wanalalamikia kwamba yamekaa idle na watu hawaendelezi lakini ukiangalia taratibu za kuanza kufuta ukienda kwenye Sheria Na. 4 ukianzia kile kifungu cha 45 unakwenda mpaka kifungu cha 48 kuna taratibu zote zimewekwa. Kuna kumpa onyo akajibu, kuna kumwambia ajirekebishe, kuna kumpa notice yakumnyang’anya. Sasa usipofuata taratibu zile huku Wizarani hatuwezi kutoa ushauri kwa Mheshimiwa Rais kufuta, lazima taratibu zifatwe na wengine wanatoa Ilani halafu wanatulia, sasa sisi huku Wizarani au Serikalini hatuwezi kuja kukupangia wewe nani anyang’anywe wewe uliyekaa kule ndiyo Mamlaka za Upangaji wa Miji, angalia taratibu zako zote kisheria zimezingatiwa, hilo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, kuna mengine yanakuwa yana migogoro kwenye Mahakama mfano mzuri shamba la Efatha linalozungumziwa, Serikali na Mheshimiwa Naibu Waziri amelijibu pale. Lakini Serikali ilishafanya kazi yake vizuri na Mahakama ikatimizwa wajibu wake na hii ni Mihimili mitatu iliyo tofuati. Kama kuna agizo la Mahamaka sisi hatuwezi kuliingilia kwa sababu tunaheshimu ule Muhimili. Lakini bado tulifanya mazungumzo na wenzetu wa Efatha na wakaridhia ekari 3,000 kutoka kwa ajili ya kugawia vile vijiji vitatu vinavyozunguka pale.

Kwa hiyo kazi inayotakiwa kufanyika pale ni zile ekari 1,000 waweze kuonyeshwa. Lakini utaratibu wa kusema unamnyang’anya kwa sababu tayari shamba lile lilipata nadhani hati yake kwenye mwaka 1997, kijiji au vijiji vimekuja kuandikishwa mwaka 2007 vimeandikishwa ndani ya umiliki wa muhusika. Sasa pale inakuwa ni vigumu vinakinzana katika namna vyote vimetoka Serikalini halafu wananchi wanabaki wanaangalia. Lakini kwa kuona tatizo hilo ambalo tayari lilionekana ndiyo maana Serikali ilichukua uamuzi wa kuzungumza naye ili aweze kuridhia ekari 3,000 zitolewe wananchi wapewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hii inakuwepo kwa sababu tu namna ambavyo tunaishi kule katika maeneo na wawekezaji na namna ambavyo wawekezaji wasivyokuwa waaminifu katika kutimiza masharti ya hati wanazozimiliki. Kwa hiyo, ndiyo changamoto kubwa ambayo sasa Wizara yangu itaendelea kuangalia kwa kina na naagiza katika kikao hiki Halmashauri ambazo ni Mamlaka za Upangaji fanyeni ukaguzi wa maeneo yote ambayo wawekezaji wamepewa na muangalia masharti yake kama yametimizwa kama hayajatimizwa taratibu za kuwanyang’anya zianze kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tutakapokuwa tumewanyang’anya kwa mfano kwenye mashamba tusikimbilie kupanga viwanja, kuna maeneo wanataka kwa ajili ya kupanga tukipanga viwanja maana yake tutajikuta tunakosa hata maeneo ya kilimo. Kilimo cha mjini kinakubalika, kwa hiyo chukua eneo, panga maeneo yako kama yameshavamiwa na watu tutapanga makazi ambayo hayajavamiwa basi wekeni kile kilimo cha mjini ili walau wananchi waweze kupata maeneo ya kuendelea kuwa na kilimo. Sasa leo ukimnyang’anya mmiliki aliyekuwa analima, halafu wewe ukaweka majengo tu maana yake utakuwa hujaisaidia Serikali. Kwa hiyo, naomba kusema kwamba taratibu zizingatiwe na tuone jinsi ambavyo tunafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Mheshimiwa Mwita Waitara ambalo amelizungumzia eneo lake ambalo amelisema la Kijiji cha Komarero ambalo lina jumla ya ekari 652 tayari katika eneo lile lina wananchi 6,847 tathmini ilishafanyika na fidia imeshalipwa kwa watu 1,515 kati ya hao 6,847. Na katika kijiji kingine ambacho amekitaja cha Kewanja tayari kazi ya tathmini inaendelea kule, tatizo linalokuja ni katika lile eneo ambalo mwekezaji alitaka kulichukua akiwa na mawazo ya kuwa na ile open pitch process za kuchimba, baadae akabadilisha mawazo akasema anakwenda kwenye underground, akaamua kuacha. Serikali hatujakaa kimya tumefanya mazungumzo naye ili aone namna gani, kwa sababu wananchi wale walisimama kwa muda mrefu kuweza kuendeleza maeneo yao kwa sababu alionesha nia ya kulichukua. Lakini kashindwa kulichukua pengine kwa sababu amebadilisha, badala ya kuwa na open pitch sasa anakwenda na underground kwenye uchimbaji wa madini.

Kwa hiyo, tumemtaka pengine aweze kuona namna ya kulipa walau fidia kidogo kwa wale aliowachelewesha, lile amelichukua na amepeleka kwa mshauri wake anasubiri kushauriwa namna ya ambavyo ataweza kuwalipa kwa sababu kosa ni la kwake na siyo la wananchi amewachelewesha katika maendeleo yao. Kwa hiyo, hayo yote yanafanyika kwa kuangalia ni namna gani tunaweza kusuluhisha haya mambo yaweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, wamezungumzia suala la kupanga, kupima na kumilikisha na hiyo ndiyo hoja ya msingi zaidi pengine ningetaka Waheshimiwa Wabunge tuichukue vizuri na tuone namna gani tunafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yetu ni Wizara ambayo inasimamia, inatunga sera, Miongozo mbalimbali kwa ajili ya kusimamia katika taaluma yake au sekta ambayo inaiongoza. Mamlaka za Upangaji zote ni Halmashauri kwa mujibu wa Sheria Namba 8 ya Mipango Miji ya mwaka 2007. Takwa hili la kisheria si mamlaka zote za Halmashauri zinalitekeleza Serikali imeingilia kati kutaka kuongeza ile kasi pengine ya upimaji ili kupunguza malalamiko ya wananchi na ndiyo maana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan tunamshukuru sana kwa kutoa ile shilingi bilioni 50 ambayo tumekwenda kuikopesha katika Halmashauri 55 lakini kuna pesa nyingine ambayo imetoka bilioni tano ambayo imekwenda kufanya kazi ile ile. Lengo letu ni kutaka kusaidia kusukuma kwenye mamlaka husika ambayo ndiyo hasa inayotakiwa kufanya kazi ya upangaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa baada ya Wizara kusaidia mamlaka zote zimetulia kama vile ile ni kazi ya Wizara. Mkitulia na kuachia Wizara maana yake ni kwamba tutachelewesha wananchi kuweza kupata umiliki ya maeneo yao na kuwajengea uwezo kiuchumi. Ninyi wenyewe hapa mmesema sekta ya ardhi ni sekta ambayo tukiweza kuisimamia vizuri itakwenda kunyanyua uchumi wa kila Mtanzania. Lakini tunaisimamiaje kama hatuwezi kuwamilikisha wananchi na kuwapa uwezo wa kutumia miliki zao kwenda kukopa benki.

Kwa hiyo niwatake sana Mamlaka za Upangaji watimize takwa lao la Kisheria sisi kama Wizara tutaendelea na ule mfuko ambao tulikuwa tukiutumia katika kukopesha bado tumeendelea kumuomba Mheshimiwa Rais kwamba tuweze kurejeshwa ili tuongeze ile nguvu ambayo tunaweza kusaidia. Rai yangu kwa Halmashauri zinapewa pesa Wakurugenzi wanatumia tofauti, niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwa sababu ni sehemu ya Baraza la Madiwani mnapokuwa kwenye vikao watakeni Halmashauri zenu wawaoneshe matumizi ya pesa waliyopewa kwa ajili kupanga, kupima na kumilikisha ili tuweze kuona ile kasi tunaenda pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo tunawataka pia kumekuwa na changamoto pengine ya pesa tunasema wanapouza wanakuwa na pesa nyingi za kutosha, basi katika zile pesa wanazozipata waweze kugawa kulingana na madaraja ya Halmashauri zetu. Watenge kati ya asilimia 40 mpaka 60 ya pesa zile wanazozipata faida kwenye mauzo zikaendeleze sekta ya ardhi badala ya kuzitumia kwenye matumizi mengine. Tukifanya hivyo tutajikuta kasi imeongezeka na tunatambua sana katika suala hili kama Halmashauri zingeweza kutenga walau vijiji au hasa vijiji vitano, 10 kila mwaka tungeweza kusogea mbele. Lakini hawafanyi kazi hiyo wanaangalia Tume, Tume iko kwa ajili ya kuwezesha katika kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo Tume inaingia pia katika suala zima la kupanga mpango mzima wa matumizi ya ardhi ikiwa pia ni kuhakikisha Halmashauri zinajengewa uwezo kupitia zile Kamati zake waweze kuendelea na hili zoezi.

Kwa hiyo, mimi niwaombe Halmashauri waone kwamba hili pia ni jambo la msingi kama Serikali tunatakiwa kulifanya kwa pamoja ili tuweze kuona tunakwenda namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika masuala mengi ambayo yamezungumzwa limezungumzwa suala la hatimiliki za kimila kuweza kukopa benki. Naomba niseme tu kwamba tunao mfano mzuri Halmashauri ya Mbinga, Bariadi, Babati na nyinginezo ambazo zimetumia hatimiliki za kimila kuweza kukopa benki, tatizo lililopo tu hapa ni la kisheria ambalo kama Mheshimiwa Kakunda alivyosema tutakwenda kuiangalia sheria. Kwa sababu hairuhusu mtu mmoja anapojisikia kwenda kupima aende apime, lazima mamlaka zinazohusika ziweze kufanya kazi hiyo.

Kwa hiyo tutaiangalia ile sheria tuweze kuona ni jinsi gani tunaweza tukaweka utaratibu ambao utaongeza kasi ya kumiliki, kwa sababu sasa hivi mtu akitaka kupima anaambiwa pengine apime na wanakijiji wenziwe wote kitu ambacho kinakuwa ni gharama ambacho pengine yeye hawezi. Lakini kama Halmashauri zetu zingefanya kazi hiyo zingeweza kutusaidia sana. Kwa hiyo mimi niombe tu hayo yaweze kufanyika ili tuweze kuona ni jinsi gani tunakwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la uwekezaji limezungumzwa hapa Mheshimiwa Chumi amezungumza na nimpongeze kwa kutenga eneo la industrial park sisi kama Wizara tayari tumeshatenga hekta 224,000 tukiwa tumejiweka tayari kwa sababu tunafahamu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan ameshatuelekeza, Wizara iwe tayari wawekezaji wanapoingia maeneo yawepo. Niwaombe tena Mamlaka za Upangaji, Mamlaka ambazo zimeshaandaa mipango kabambe kwa ajili kutenga maeneo kwa matumizi hakikisheni maeneo yale yanakuwa na umiliki either imilikiwe na Halmashauri au imilikiwe na Halmashauri ya Kijiji au Halmashauri yenyewe kwa maana ya kwamba mwekezaji anapopatikana asianze tena kusubiri mchakato wa uhaulishaji kama ni eneo la kijijini, lakini kama ni la mjini basi tujue umiliki uko kwa nani ili mwekezaji anapokuja anakwenda moja kwa moja tayari kwa mmiliki na wanakubaliana namna ya kulitoa lile eneo. Mwekezaji akija mpaka twende kijijini tuweke vikao tunachelewesha kitu ambacho Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan hataki kusia hayo. (Makofi)

Kwa hiyo mimi niwaombe sana katika hili Mamlaka za Upangaji zione haja ya kuona ni jinsi gani tatakwenda kutatua tatizo hili kwa sababu tunajua ni hitaji nchi imefunguka na wanahitaji kuwa na wawekezaji wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mengine nitayaruka lakini nizungumzie suala la National Housing; limezungumzwa suala la nyumba zimechoka ni kweli nyumba nyingi, lakini tukumbuke mwaka jana tuliripoti hapa walikuwa wameshaweka mpango kwa ajili ya kufanya ukarabati na walitenga shilingi bilioni nane kwa ajili ya kuendelea kufanya ukarabati katika majengo yao 300 ambayo hasa yapo katika Mkoa ya Kilimanjaro, Mtwara, Katavi na Tabora itaingia katika mwaka huu wa fedha. Ni kweli yako yamechoka, lakini tunaamini, mmempongeza pia na Mkurugenzi Mkuu ninaimani kwa usimamizi wake atakwenda kufanya kazi yake vizuri. Na majengo yale ya uwekezaji ambayo yamezungumzwa yalikuwa yamesimama kwa muda mrefu tayari Serikali ilisharidhia ili waweze kuendelea kuyakwamua na kuendelea kuweza kuendelea nayo kama kitega uchumi. (Makofi)

Kwa hiyo, tusema haya yote tunayachukua tukitambua ya kwamba tupo pamoja katika kuhakikisha kwamba kila ambalo mnaelekeza, kila ambalo mnashauri tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru sana Kamati ya Kudumu ya Ardhi, Maliasili na Utalii wameelekeza mambo mengi ushauri wao wameutoa tumeupokea kwa jinsi walivyoutoa, lakini niwahakikishie tu siku zote tumekuwa tuko pamoja katika hili. Tuzungumzie suala la kutofikia malengo katika ukusanyaji, kama ambavyo property tax iliingia kwa watoaji huduma sisi Wizara tunataka pia kuzungumza na watoa huduma kama wa maji ama TANESCO. Mtu ambaye anayetakiwa kulipa kodi pengine ya 300,000 kwa mwaka ukiagawa kwa miezi 12 utasikia ni kidogo sana. Kwa hiyo, tunajaribu kuangalia namna itakavyokuwa mbali na hiki ambacho amekizungumza Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba ile mifumo yetu pia itakwenda kuongeza kasi ya makusanyo. Lengo la Serikali ni kuhakikisha tunawezesha mfuko mkuu wa Serikali kupata kile ambacho Mheshimiwa anakihitaji. Tusipo…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa toa hoja.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

NAIBU SPIKA: Umejibu vizuri sana, toa hoja. (Makofi/Kicheko)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba tumeyachukua, tutayafanyia kazi, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja na kuwapongeza kwa kazi nzuri katika Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni Mkoa wa Mwanza pamoja na kuwa makazi ya makabila zaidi ya manne, lakini Wasukuma ni wengi zaidi. Kuna utamaduni wa Kisukuma ambao umejengeka na kuhifadhiwa kwa njia ya ngoma na vitendea kazi vilivyokuwa vinatumika enzi za mababu zaidi sana historia ya uchifu kwa koo tofauti za Wasukuma umehifadhiwa vizuri.

Aidha, namna ya maisha waliyoishi na kuweza kudumisha amani ya maeneo yao lakini pia Kituo cha Bujora kimetunza kumbukumbu zote vema ambapo watalii wanaweza kutembea na kujifunza mengi. Rai yangu naomba Kituo cha Bujora kiingizwe katika maeneo ya vivutio vya utalii nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ziwa Victoria mbali na kuwa ziwa la pili kwa ukubwa duniani bado halijatangazwa vema, tunaweza kutangaza kivutio hiki kwa kuwekeza katika michezo ya ziwani kwa kuweka sports boats (speed boats) ambapo watalii wanaweza kushiriki kikamilifu. Aidha, wanaweza kufanya uvuvi (sport fishing) ambapo Ziwa Victoria ni tulivu, uvuvi wa aina hiyo ya utalii unaweza kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa uwanja wa ndege wa Mwanza upo katika upanuzi, bado watalii wanaweza kutumia uwanja huo kwenda Serengeti ambapo ni karibu zaidi tofauti na KIA ambako ndiko watalii wengi wanapitia.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja na niwapongeze kwa kazi nzuri pamoja na changamoto zote wanazokumbana nazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nishauri tu katika kuboresha sekta ya uvuvi ni vyema season fishing ikapewa kipaumbele, italeta tija sana katika sekta hii. Tuyatambue mazalia ya samaki na kisha tuweke programu maalum ya kutekeleza season fishing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tutoe kipaumbele katika cage fishing. Tuwekeze kwa vijana ili ufugaji wa samaki ufanyike katika mfumo wa kuwa na plot ndani ya ziwa ama bahari kwa kuweka wigo katika maeneo yatakayowekezwa katika uvuvi kwa njia ya uvuvi wa wigo ziwani ama baharini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kuhusu ufugaji wa ng’ombe ni vyema wafugaji/wachungaji wakashauriwa kufuga ufugaji wa kitaalam na kuwaelekeza wafugaji wetu kufuga kitaalam ili wawe na tija katika ufugaji wao badala ya kuwa na ufugaji wa kuhamahama kitendo ambacho kinachangia sana katika kuleta migogoro ya wakulima na wafugaji.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa kupata fursa hii na niwapongeze pia Kamati kwa kazi nzuri waliyofanya. Ninazo hoja mbili tu ambazo nataka kuchangia kutoka kwenye hii Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Jambo la kwanza, linapatikana kwenye ukurasa wa 21 inalozungumzia suala la alama za mipaka. Suala hili kidogo limekuwa na tatizo na changamoto lakini nilitaarifu Bunge lako kwamba sasa Wizara imepata pesa tumepewa bilioni nne kwa ajili ya kuhakiki mipaka hiyo na kazi zinazokwenda kufanyika ni kukarabati zile pillars zote za zamani ambazo zimechakaa lakini pia na kuweka pillars mpya ambapo hapakuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu pia zilikuwa na umbali mrefu sasa hivi tutakwenda kuweka umbali wa mita 100 kutoka pillar moja mpaka nyingine ili iweze kuonekana na hii inakwenda kufanyika kwenye mpaka wa Tanzania na Uganda pamoja na mpaka wa Tanzania na Kenya kazi hizo zinaenda kufanyika.

Lakini pia kazi nyingine itakayofanyika ni kuwa na ile ramani ya msingi kwa maana ya base map ili kuweza kutambua vilivyoko pale ardhini ikiwa ni pamoja na kusafisha ule Mkuza ulioko pale, kazi hiyo inakwenda kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapakuwa pia na protocol ya mpaka pale itakwenda kufanyika mwaka huu kwa sababu pesa tulizokuwa tumeweka kwenye bajeti zote zimetolewa na tunaishukuru Serikali kwa kazi hiyo.

Jambo la pili, ni mgogoro wa mipaka ambao umekuwepo katika taasisi nyingi za Jeshi.

Napenda kushukuru sana Wizara ya Ulinzi ambayo iliunda kamati ambayo imepitia katika mipaka mingi inayohusiana kati ya Jeshi na wananchi na wamehakiki mipaka yao yote na maeneo ambayo walikuwa wakiyahitaji wanaendelea nayo na yale ambayo walikuwa hawayatumii na hawayahitaji basi yale watakuwa wameyarejesha baada ya kuwa wameshakamilisha taarifa yao. Lakini kubwa zaidi ni kuzikumbusha taasisi zote...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
Muswada wa Sheria ya Uthamini na Usajili wa Wathamini wa Mwaka 2016
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru kabisa kwa kunipa fursa ya kuja kutoa mchango wangu lakini wakati huohuo kuweza pengine kujibu baadhi ya hoja ambazo wachangiaji wamezisema. Napenda tu nianze kwa kuwashukuru wachangiaji wote ambao wametoa hoja zao tukianza na Waziri mwenyewe mtoa hoja, Mwenyekiti wa Kamati na Mwakilishi wa Kambi ya Upinzani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wote katika taarifa zao wamesema vizuri na karibu sehemu kubwa wanaunga mkono Muswada huu. Pia wachangiaji wote kila aliyesimama alikuwa anapongeza maana yake ni kwamba Muswada huu umekuja wakati muafaka ambapo pengine imekuwa ni kero ya muda mrefu, lakini sasa ndiyo muda wake wa kuweza kuitungia sheria ili wanataaluma hawa waweze kufanya kazi zao kwa weledi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kupitia hoja za Waheshimiwa Wabunge ambazo wamezitoa na zile ambazo pengine sitazizungumzia hapa basi nina imani Mheshimiwa Waziri atakuja kuzizungumzia. Msemaji wa kwanza Mheshimiwa Sabreena alizungumzia suala la uteuzi wa Mthamini Mkuu akasema usifanywe na Mheshimiwa Rais. Hata hivyo, tunasema kwamba kutokana na uzito na umuhimu wa nafasi yenyewe bado kama Serikali tunaona ni muhimu Mheshimiwa Rais aweze kuteua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo tumepanua wigo badala ya kuteua kutoka ndani ya watumishi wa umma peke yake anao pia wigo mpana wa kuweza kuangalia pia hata walioko nje ya Serikali. Kwa maana hiyo, bado kuna nafasi kama kuna Mthamini aliyebobea nje ya Serikali kwa maana ya mtumishi wa umma basi atapata fursa hiyo. Jedwali la Marekebisho limepanua wigo huo na nadhani litakuwa limeshapita huko na mtakuwa mmeliona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia akazungumzia uzoefu wa Mthamini Mkuu kuwa wa miaka 10 kuwa ni mingi sana hivyo kusababisha pengine vijana kukosa nafasi hii. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge niseme nafasi tunayoizungumzia ni ya Mthamini Mkuu na ni nafasi moja. Sasa ukimpa muda mfupi wakati nafasi hii ni nyeti na Taifa linamtegemea zaidi katika zoezi la uthamini haitakuwa sawa. Ukipunguza miaka hii na sisi tunahitaji mtu mwenye weledi mkubwa na nafasi yenyewe ni moja, kidogo tutakuwa hatujatenda haki sawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunasema kwamba kutokana na umuhimu wa nafasi yenyewe na majukumu ya Mthamini Mkuu wa Serikali jinsi yalivyo anahitaji kuwa na uzoefu wa kutosha ili kuweza kusimamia eneo hilo, uzoefu ni kigezo cha yeye kupewa nafasi hiyo. Sasa anavyosema vijana watakosa ajira au muda ni mwingi bado tunasema kwamba ile nafasi inahitaji mtu aliyebobea katika nafasi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwenye suala la usajili, kigezo cha uzoefu wa miaka mitatu Mheshimiwa Sabreena alipendekeza ipungue iwe mwaka mmoja. Ili mtu aweze kusajiliwa kuwa mthamini ni lazima awe na uzoefu wa kutosha wa kumudu majukumu yake. Sheria inayopendekezwa imepunguzwa muda kutoka miaka mitano na kuweka miaka mitatu. Tukumbuke pia tuna taaluma zingine kama za wenzetu watu wa CRB ambazo pia ni taaluma kama hii ambayo tunakwenda kuizungumzia, hizi ni rare professional, tunahitaji watu ambao wamefanya kazi kwa weledi chini ya watu na wamesimamiwa na wanaweza wakajisimamia wenyewe baada ya kuwa wamepata uzoefu wa kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tulipunguza kutoka kwenye hiyo miaka mitano na kuleta mitatu baada ya wajumbe ndani ya Kamati pia kusema kwamba huu ni muda mwingi sana. Sasa ukiupunguza ukawa mmoja maana yake pia tunakuwa hatujapata yule mtu tunayemtaka na tukumbuke kazi hii ni kazi ambayo imeleta migogoro mingi sana na bado kuna migogoro mingi kwa hiyo, hatuhitaji kufanya majaribio katika hili. Mfano, nimetoa kwa wenzetu hawa wa engineering registration, nao wanakwenda kwa miaka mitatu na hii ni rare professional. Kwa hiyo, kwa nini tunasema miaka mitatu na siyo mwaka mmoja ni kutokana na unyeti wa kazi yenyewe wanayokwenda kufanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Sabreena amezungumzia pia suala la kwamba wazawa hawakupewa kipaumbele au kutiliwa mkazo bali wageni ndiyo wamependekezwa. Nadhani katika pendekezo hili kifungu cha 25 kwenye huo Muswada kimetoa muda wa mtu asiye mzawa kutokana na kazi anayoifanya ambayo ni ya muda usiozidi mwaka mmoja, ana limit ya kufanya kazi hiyo siyo kwamba wamependelewa. Vilevile leseni anayoipata ni ya mwaka mmoja tu, baada ya hapo tena hatuko naye. Kwa hiyo, hakuna upendeleo isipokuwa tumejaribu kuweka muda wa mwaka mmoja kwa wale ambao siyo wazawa wa hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameuliza Muswada wa Uthamini utakavyodhibiti hasara iliyosababishwa na wathamini. Katika kifungu cha 67 cha Muswada huu kimeorodhesha adhabu kutokana na makosa mbalimbali ya uthamini na hasara iliyofanywa kwa vitendo na mthamini. Kwa hiyo, tuna imani kama wataisoma sheria vizuri siyo rahisi kwenda kinyume na kile ambacho kimepangwa na ndiyo maana na adhabu zake ni kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Elias Kwandikwa yeye amezungumzia mkanganyiko uliopo katika Ibara ya 26 na 27 katika suala zima la usajili. Tunachosema hapa ni kwamba sheria hii inasomeka sambamba na sheria nyingine, hivyo lazima hizi sheria tuziangalie. Unapoangalia vigezo vilivyowekwa huyu mwingine ni mtu aliyesajiliwa lakini mwingine ni mtu ambaye bado yupo kwenye practical anahitaji kusajiliwa, yupo katika matazamio, kwa hiyo, huwezi kuwalinganisha katika makosa yao. Huyu mwingine yupo full registered na tayari ameshaanza ku-practice, huyu mwingine anajitangaza tu bado hajaweza kupata ile full registration ya kuweza kufanya kazi hizo maana yake akifanya kosa lile anapewa adhabu. Kwa hiyo, adhabu za hawa watu wawili haziwezi kulingana, lazima yule mmoja ambaye anatambua sheria inaambana namna gani akifanya kosa lazima adhabu yake iwe kubwa kuliko huyu mwingine ambaye anajitangaza kwamba yupo kati ya wale wathamini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chumi yeye amezungumzia Ibara ya 20 na 21 haisemi adhabu gani itatolewa kwa watakaokiuka maadili ya sheria iliyopendekezwa. Adhabu zote zinatokana na taaluma ya uthamini na zimeainishwa katika Ibara ya 67 kama nilivyozungumza hapo juu, kimeorodhesha adhabu zote kulingana na kosa alilofanya. Kwa hiyo, hapa hakuna mkanganyiko wowote ambao upo, hasara itakayofanyika pale lazima itakwenda sambamba na ukiukwaji wa maadili ya taaluma, ataadhibiwa kwa mujibu wa Ibara ya 67.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameomba pia Muswada uweke kifungu kitakachoweka haki ya mlalamikaji. Utaratibu wote kuhusu malalamiko dhidi ya Wathamini waliosajiliwa utaainishwa katika kanuni. Ukitaka kuweka kila kitu katika sheria tungekuwa na Muswada mkubwa sana ambapo sasa inakwenda kutokea sheria ambayo imejaa mambo mengi, lakini kuna mambo mengine ambayo yataainishwa kwenye kanuni. Kwa hiyo, hayo anayoyazungumzia yatakwenda kuonekana katika kanuni zitakapokuwa zimeandaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumzia pia Ibara ya 8 kuhusu Wathamini Wakuu Wasaidizi ambapo anapendekeza wawe na shahada moja na uzoefu wa miaka mitano isiwe sawa na sifa ya Mthamini Mkuu. Tukumbuke huyu Mthamini Msaidizi atakwenda kufanya kazi katika Ofisi za Kanda na tunatarajia atafanya kazi sawasawa na zile anazofanya Mthamini Mkuu aliyeko pale Wizarani. Kwa hiyo, ili aweze kufanya kazi yake vizuri na kwa uhakika ni lazima na yeye sifa zake zifanane na yule Mthamini Mkuu kwa sababu kule kwenye kanda atafanya shughuli zote za uthamini kulingana na majukumu atakayokuwa amepewa. Kwa hiyo, ukisema yeye awe na sifa za chini kidogo maana yake tutakuwa tunazishushia pia hadhi kanda zetu ambazo tumesema tuna kanda nane na kila kanda itafanya kazi zote kama ambavyo zitafanywa Wizarani. Kwa hiyo, bado sifa ya yeye kuwa sawasawa na Mthamini Mkuu tunasisitiza ni muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chumi pia ameongelea suala la Ibara ya 68 Mthamini Mkuu awajibike kwa uzembe wa kitaalam utakaosababishwa. Mthamini Mkuu kwa makosa ya kitaaluma atawajibishwa na Bodi na ndiyo maana katika uundaji wa Bodi pia wao watakwenda kuweka kanuni (rules) ambazo zinawasimamia hawa wathamini. Kwa hiyo, yeye adhabu yake itatokana na Bodi ambayo imemsajili na katika utendaji wake wa kazi yupo chini ya Bodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumzia suala la utata wa ukomo wa muda pale ambapo siku itakapoanza kufanyika maendelezo au katika muda wa miaka miwili iliyoelekezwa toka siku ya kujaza fomu na ni lini kipindi hicho kitaanza kuhesabika. Tumesema kipindi kitahesabika baada tu ya taarifa ya mthamini kuidhinishwa na Mthamini Mkuu wa Serikali, hapo ndipo tunapohesabu ile miaka miwili. Baada ya hiyo miaka miwili kwisha kama bado malipo ya fidia hayajafanyika maana yake ule uthamini tena hauhesabiki, utakwenda kuanza uthamini mwingine mpya lakini kwa kuzingatia ile hali halisi iliyokuwepo kwa wakati huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama viwango vya malipo vitakuwa vimebadilika, basi tutachukua vile vilivyopo lakini kwa kuangalia ile hali halisi iliyokutwa wakati uthamini wa kwanza unafanyika. Hapatakuwa na zoezi la kurudi kule site kufanya uthamini upya isipokuwa uthamini ule ule uliofanyika mara ya kwanza ndiyo huo huo utakaorudiwa tena, lakini kwa kutumia viwango vipya ambavyo vimewekwa katika utaratibu wa bei zile za fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chumi kaongelea pia suala la notice kabla ya mthamini hajaingia kwenye eneo la wananchi na nini kifanyike. Tuseme hili limezingatiwa kwenye Jedwali la Marekebisho katika Ibara ya 55(1).
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Sophia Simba yeye ameongelea habari ya elimu itolewe kwa wananchi kuhusu haki zao juu ya sheria hii. Serikali inasema tumezingatia ushauri huu na utakwenda kufanyika kwa sababu kwa vyovyote vile unapokuwa na sheria mpya ni lazima pia elimu itolewe ili watu waweze kutambua. Kwa sheria hii kila mmoja nadhani atakuwa anaisubiri kwa hamu kwa sababu tayari watu wameumizwa sana, watu wamelia sana. Kwa hiyo, ushauri wake tumeuzingatia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwenda Ilala ili kuweza kumaliza tatizo nalo tumelizingatia tutalifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia amezungumzia sheria zinazogusa masuala ya uthamini zihuishwe ili kuondoa masuala ya mgongano. Hili nalo tumelizingatia katika Jedwali la Marekebisho katika Ibara ya 72.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Hamidu Hassan Bobali yeye amezungumzia tafsiri ya property kwamba iongezwe baadhi ya maneno. Tafsiri inayopendekezwa haitofautiani sana na iliyopendekezwa kwenye Muswada. Hivyo Ibara ya 2 imetoa tafsiri kwamba ni mali zinazohamishika na zile zisizohamishika na aina za mali ambazo zinafanyiwa uthamini na pia inakuwa imezingatia matakwa ya tafsiri ambayo imependekezwa. Kwa hiyo, imeguswa hatuhitaji pengine kuweka ufafanuzi mwingine zaidi ya ule ambao upo kwa sababu unapozungumzia mali zinazohamishika na zisizohamishika tayari unakuwa umegusa aina nyingi ya mali ambayo ipo pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumzia pia suala la ugatuzi wa madaraka katika huduma inayotolewa na Mthamini Mkuu iwe inapatikana hadi vijijini kwenye Halmashauri. Muswada unaopendekezwa Waheshimiwa Wabunge umezingatia suala hili katika Ibara ya 10, kutakuwa na Wathamini Wateule katika kila Halmashauri. Hawa wathamini siyo kwamba watakuwa chini ya Wizara ni sawasawa na kwenye Halmashauri zetu ambapo tunao Maafisa Ardhi Wateule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo na kule kutakuwa na Mthamini Mteule kwa sababu Wathamini watakuwepo wengi, lakini lazima wawe na kiongozi wao ambaye atakuwa anawajibika pia katika kutia saini zile fomu za uthamini unapokuwa umefanyika uthamini. Kwa hiyo, hawa wapo kule kwenye Halmashauri siyo kwamba watakuwa Wizarani. Kwa hiyo, hili limezingatiwa pia katika muundo mzima ulivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 52 kuhusiana na ukomo wa miaka mitatu ni mingi. Jedwali katika Ibara ya 52 limerekebisha na tumezungumzia miaka miwili kama hapo juu nilivyozungumzia nini kinakwenda kufanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Richard Phillip Mbogo yeye anasema hajaona kifungu cha kukata rufaa kwa mtu ambaye hajaridhika. Sheria hii siyo kwamba itakwenda kusimama peke yake bali itakwenda kusomwa sambamba na sheria zingine na Sheria ya Ardhi imeweka utaratibu wa ukataji rufaa kwa watu ambao hawajaridhika na uthamini. Kwa hiyo, sheria hii siyo kwamba inakwenda kusimama peke yake. Katika maeneo ambayo pengine hayakutajwa hapa, basi kuna sheria ambayo inakwenda kugusa wapi mtu anaweza kwenda kukata rufaa au kulalamika pale ambapo anakuwa hajatendewa haki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 57, Mheshimiwa Phillip amezungumzia habari ya kwamba inaipa Bodi mamlaka makubwa na kufanya Bodi kusema itakavyo. Kwa hiyo, yeye anashauri kanuni ya Waziri itaje adhabu ambazo Bodi itazitoa. Muswada huu umefafanua taratibu na mamlaka kati ya Bodi na Waziri, kwa hiyo, hilo litazingatiwa katika utaratibu huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumzia Ibara ya 49 anasema sababu za kufanya uthamini ziwe standard na zitajwe katika kanuni zitakazotolewa na Waziri. Waheshimiwa Wabunge Ibara ya 49 imetaja madhumuni mbalimbali ya uthamini yanayotambulika kitaaluma. Kwa hiyo, haya yote yameorodheshwa na yatakwenda kufanyika kulingana na sheria itakavyokuwa, hatuhitaji tena kutaja moja baada ya nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Pauline Gekul yeye amezungumzia kwamba Wakuu wa Wilaya hawakutajwa. Hili litazingatiwa katika kanuni kwa sababu hata ile ya awali walivyokuwepo walikuwa wametajwa katika kanuni, hawakutajwa katika sheria. Kwa hiyo, bado wapo watafanya kazi zao, lakini watatajwa kwenye kanuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, akauliza kwa wananchi ambao bado hawajalipwa fidia mpaka leo sheria hii ikishapita hatma yao ni ipi? Sheria hii itaanza kutumika pale itakapokuwa imetangazwa, kwa hiyo, kwa ile migogoro mingine yote ya nyuma ambayo ipo sasa, sheria ya zamani iliyopo itaendelea au tuseme sheria zilizopo za ardhi bado zitaendelea kusimamia hilo. Kwa hiyo, hapatakuwa na hitaji lolote la kuweka pale kwa sababu kuna sheria. Kama kuna mtu pengine anaona kwamba hajatendewa haki basi itashughulikiwa kwa njia ya kimahakama, anaweza akachukua hatua ya kwenda kulalamika lakini bado anaweza akatendewa haki kwa mujibu wa utaratibu huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 7(2)(a), anasema kifungu kitaje aina ya adhabu. Hii imezingatiwa katika Ibara ya 67 ambayo imeainisha adhabu mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumzia ukomo wa mwaka mmoja, hii imezingatiwa katika Ibara ya 52 ambapo tumetaja miaka miwili na siyo mmoja kama ambavyo anapendekeza na nimeshaliongelea hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, akauliza endapo mtu alichukua ardhi kwa ajili ya maendelezo akaamua kuiachia ardhi hiyo nini hatma yake. Tunasema basi endapo mtu alisimamishwa kuendeleza shughuli zake halafu mtu akaamua tena kusema kwamba hafanyi tena hii kazi, akaamua kuachia basi huyu mtu anayo haki pia ya kushtaki kwa maana kwamba sheria zingine zitachukua hatua. Kwa sababu ni kitu ambacho alikisema anataka kukichukua halafu kaacha kuchukua na huyu kamkwamisha katika maendelezo yake na katika shughuli zake, basi anayo haki pia ya kulalamika katika vyombo vya sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezingatia yale yote aliyoyazungumza Mheshimiwa Maufi, nadhani amezungumzia Ibara ya 52 ukomo wa miaka, akazungumzia suala la Wathamini Wasaidizi kuepusha migogoro lakini kazungumzia pia suala la CV aliyepo, yeye anadhani anatosha. Basi vyombo vinavyohusika kwa uteuzi vitakuwa vimesikia kilio chako pengine inaweza ikawa kama unavyoomba lakini tuseme Inshallah Mwenyezi Mungu atabariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Omary Mgumba naye kazungumzia Ibara ya 52 ambayo tayari tumeshalizungumzia. Katika suala la CV kukaa na ule uthamini, tumesema ikishafika kwa CV haitakiwi izidi siku saba na itawekwa kwenye kanuni kwa sababu ni lazima izingatiwe kwa maana kama kazi yote imeshafanyika kazi yake yeye ni kujiridhisha, hatutarajii kwamba atakaa nayo muda mrefu. Kwa hiyo, ndani ya siku saba lazima awe amemaliza na ameitoa kwenda kufanyiwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Silinde ameongea mambo mengi ambayo yana ushauri pia tunashukuru lakini kwa suala la uthamini kufanywa na makampuni mawili hilo ni kosa, hakuna mahali ambapo makampuni mawili yatafanya uthamini kwa wakati mmoja halafu useme ni uthamini umefanyika, hilo ni kosa tayari. Hiyo inaweza ikafanyika pengine kuona kwamba kuna kitu hakikwenda sawa, mtu ame-appeal basi inateuliwa kampuni nyingine au watu wengine kwenda kufanya lakini haiwezekani wathamini kutoka makampuni mawili kufanya kazi moja halafu tulinganishe kazi zao nani kasema vipi, hilo ni kosa pia katika taaluma ambayo wanakwenda kuifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini akasema anataka kujua pia thamani ya nyumba kabla ya mambo ya uthamini kuendelea. Tukumbuke kwamba unapotaka kujenga nyumba kuna mtu anayeitwa Quantity Surveyor ambaye anakuwa ameshaonesha kwenye bill of quantity. Kwa hiyo, masuala ya bill of quantity yale yale ndiyo yatakayokuwa yamechukuliwa kama thamani ya kile ambacho kimejengwa pale kwa maana ya nyumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Japhet Hasunga yeye amezungumzia muda, tayari tumekwishalizungumzia. Pia mengi aliyoyazungumzia masuala ya Bodi kujulikana kabla na kadhalika mengine yatazingatiwa kwenye kanuni kwa sababu huwezi kuya-mention yote kwa wakati mmoja. Kwa hiyo, katika hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge sehemu kubwa tumezizungumzia kwa sababu karibu yote yanajirudiarudia katika maeneo yale yale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Salma Mwassa kwa kuchangia na ameonesha Mheshimiwa ni mbobezi katika taaluma hiyo kama Mthamini na ali-declare interest na tumepokea ushauri ambao ameuzungumza. Pia napenda tu kumfahamisha yale aliyopendekeza tayari Jedwali la Marekebisho limeshayazingatia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muundo wa Bodi amesisitiza kutaja habari ya wanne kwa watano lakini hakusema sasa wanne ni wanawake au wanaume, kasema tu nne kwa tano, kwa hiyo, inaweza ikawa wanawake watano wanaume wanne. Niseme hili ni katika zile barua za kutaka yale mashirika au zile taasisi kuleta majina yao. Kwa hiyo, Waziri anapowaandikia kuleta majina maana yake ni kwamba atakuwa ametaja pale kwamba angalau apendekezwe mwanamke lazima aseme. Unaweza ukakuta majina yaliyoletwa au yaliyopo karibu yote ni ya wanawake, tunaweza tukawa na Bodi ya wanawake watupu, tunaweza tukawa na Bodi ya mchanganyiko lakini hii pia inakwenda na sifa, lazima wawe na sifa zile zilizotajwa kwa maana lazima awe registered na anaweza kufanya kazi hii. Kwa hiyo, suala la gender litazingatiwa na linaendelea kuzingatiwa kutegemeana tu pia na qualification za watu ambao wapo. Hili tunalipokea na litafanyiwa kazi pia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mengine yalijirudia, kwa hiyo nisingependa kuyazungumzia. Suala la muda wa valuation, Mheshimiwa Mgumba alikuwa anapendekeza hizi valuation zifanyike kwa muda wa miaka miwili. Huwezi kuwa na valuation ya muda mrefu namna hii, lakini hapa pia tunaangalia na scope yenyewe ya valuation. Unaweza ukawa na magari yako mawili, matatu huhitaji kuwa na muda mrefu. Kwa hiyo, muda utakuwa-determined pia na ukubwa wa kazi yenyewe wanayokwenda kufanya. Ukiweka miaka miwili kuna mingine ambayo unakuta ndani ya siku moja imefanyika, huhitaji kuwa na muda mrefu. Kwa hiyo, hili huwezi kulipangia kwamba baada ya muda huu iwe imekwisha kwa sababu ukubwa wa kazi yenyewe pia unategemea na namna ambavyo kazi inakwenda kufanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Japhet Hasunga ameongelea habari ya taarifa kuletwa hapa kwamba miezi mitatu ni kidogo. Hilo tumeliona na tumepokea ushauri wako. Ni kweli kwa sababu unapomaliza mahesabu ndani ya miezi mitatu yanatakiwa yawe yamekwenda kwa Mkaguzi wa Hesabu. Mkaguzi wa Hesabu huwezi ukampangia muda kwamba ndani ya mwezi mmoja awe amemaliza vinginevyo hesabu zitakuja hapa hazijakaguliwa. Kwa hiyo, tumeliona hili na tumeangalia pia taasisi nyingine zinafanyaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa NIMR wana miezi sita kwa sababu tunajua kwamba ukishamaliza ndani ya miezi mitatu umepeleka kwa Mkaguzi Mkuu kule naye ana muda wake wa kufanya hesabu na siyo kwamba ana ya kwako tu na taasisi nyingine zimepeleka pale, kwa hiyo tumeweka muda wa miezi sita…
Ndani ya miezi sita tuna imani kazi ya ukaguzi itakuwa imekwisha na Waziri atapata fursa nzuri ya kuzileta hesabu hizo Bungeni zikiwa zimekaguliwa. Kwa hiyo, tumechukua ushauri wake Mheshimiwa Japhet Hasunga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Mtuka kwa sababu yeye pia ni mwana taaluma wa uthamini, ushauri alioutoa tumeuchukua tutaufanyia kazi. Sehemu kubwa ambayo amezungumzia ni pale ambapo anasema kwamba Wajumbe wa Bodi wako tisa na zipo kama Kamati nne, sasa wakiunda Kamati zile ina maana Kamati moja inaweza ikawa na watu wawili au watatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia ile Ibara ya 13 imeongelea kama Bodi itahitaji mtu pengine kwa taaluma yake kutakuwa na wale co-optedmembers kutoka nje ambaye atakuja tu pengine kwa ajili ya kutoa uzoefu wake katika taaluma fulani. Unaweza ukawa unafanya shughuli ya mambo ya mahesabu, unahitaji pengine mtu aliyebobea, kwa hiyo, atakuja kama co-opted member kuweza kutoa ushauri wake pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, habari ya kuwa na Wajumbe wa Bodi tisa hilo lipo kisheria, huwezi kusema kwamba utakuwa nao wengi zaidi ili uweze kuwa na Kamati zilizo na watu wengi, kwa hiyo, wanaweza wakawa watatu. Wala siyo vibaya mtu mmoja kuwa na Kamati mbili lakini bado wata-co-opt members kutoka nje pale wanapoona kwamba wanahitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumzia suala la exemption ya fee kwa taasisi za Serikali na hasa zile zinazofanya uthamini wa mara kwa mara. Kama Serikali tumelichukua hilo na nadhani litakwenda kuwekwa katika kanuni kwa sababu ni kweli kuna maeneo ambapo unapofanyika uthamini wa mara kwa mara unaweza ukakuta kwamba ile taasisi haiwezi kulipia hizo fee ambazo unaziweka lakini nature ya kazi yake inataka aende kwenye shughuli ya uthamini. Kwa hiyo, hili tumelichukua litazingatiwa wakati wa kuweka kanuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hoja zile ambazo zimetolewa nadhani karibu sehemu kubwa tumezizungumzia na sehemu kubwa pia zitaonekana kwenye Jedwali la Marekebisho ya Serikali ambalo limeletwa. Changamoto kubwa ambayo inakuwepo katika kazi hii na ambayo imesababisha Muswada huu kuwepo, tulikuwa na makanjanja wengi ambao wanajiita Wathamini lakini ni Wathamini hewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke pia taasisi zetu nyingi hasa za fedha zimeibiwa sana na hawa vishoka, sasa Muswada huu unakwenda kuweka nidhamu kwa taaluma husika. Kama wanataaluma wamekuwa wakitajwa na sheria nyingine na walikuwa kwenye Bodi ile ya ma-Quantity Surveyor lakini ukiangalia kazi zao zinavyofanyika wanahitaji kuwa na sheria yao ya kuwasimamia, kwa sababu sehemu kubwa pia hata Serikali imeingia hasara sana kwa watu ambao hawazingatii sheria na wakati mwingine hawana chombo kinachowabana au kinachowaongoza katika kazi yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa jinsi Muswada huu ulivyokuja tunaomba sana Wabunge wote walione hili na wote ni mashahidi huko tuliko watu wanavyolalamika, wanavyoonewa na wanavyolalamikia ule uthamini ni kwa sababu tu baadhi ya watu siyo wote walikuwa hawafanyi kazi zao kwa weledi. Kwa hiyo, inabidi kuwaweka katika mfumo ambao watadhibitiwa na Bodi yao, lakini watadhibitiana wenyewe kwa sababu pia wana association zao lakini wataheshimu ile kazi ambayo wanakwenda kuifanya. Ili waweze kufanya kazi zao kwa weledi, waweze kuheshimu taaluma yao, ni lazima kuwe na chombo ambacho kinawafuatilia na kuangalia namna ambavyo wanatekeleza majukumu yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nichukue fursa hii pia kushukuru tena kwa mara nyingine na nikiwaomba Waheshimiwa Wabunge waone umuhimu wa kupitisha Muswada huu ili tuweze kufanya kazi katika taratibu ambazo zipo kisheria na watu wanabanwa, wanaheshimu na tupunguze pia migogoro ambayo imekuwa ikiwakwaza watu wengi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja. Nashukuru na kupongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa namna ilivyotekeleza Ilani ya Uchaguzi na utekelezaji wa maamuzi magumu na yenye tija ya Mheshimiwa Rais katika kuboresha sekta ya uchukuzi kwa vitendo. Niwapongeze pia Waziri mwenye dhamana na Naibu Mawaziri wake kwa kazi kubwa na yenye tija kwa Taifa wanayoifanya kwa ushirikiano mkubwa na watendaji wao. Hongereni sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu katika miradi ya barabara, barabara ya Nyakato – Buswelu – Mhonze kilometa 18, kwa miaka mitatu mfululizo inawekwa kwenye bajeti lakini hadi sasa ni kilometa 1.2 tu imekamilika. Niombe walau kilometa 17 zilizobaki ziingie zote katika bajeti ya 2018/ 2019 ili tuondoe adha hiyo ukizingatia barabara hiyo inapita Makao ya Wilaya. Aidha, mkandarasi JASCO aliyepewa zabuni hiyo hana uwezo, ikiwezekana aondolewe. Katika bajeti imetegewa kilometa moja tu. Ninachelea kusema Awamu ya Tano itakwisha bila kukamilika barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe ukamilishaji wa matengenezo ya kivuko cha Kayenze – Base ambacho kiliwekwa kwenye bajeti ya mwaka 2017/2018 na kinaonekana tena katika bajeti ya mwaka 2018/19. Naomba ukamilishaji wake ili kusaidia wananchi wa Kisiwa cha Base.

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za Mfuko wa Barabara; matengenezo ya Sabasaba - Busweru road, tayari Halmashauri inaendelea kulipa fidia kwa wananchi. Niombe utekelezaji wake ukamilike kama ulivyopangwa ili kurahisisha mawasiliano na Makao Makuu ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa barabara za lami, mzunguko wa barabara za lami katika Manispaa ya Ilemela ni asilimia sita tu. Naomba ukamilishaji wa malengo yaliyowekwa ili hadhi ya Manispaa ilingane lingane na Manispaa zingine nchini.
Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji wa Hadhi ya Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika ili kuwa Hifadhi za Taifa. Nianze pia kwa kuwapongeza sana ndugu zetu wa TANAPA chini ya Kijaji ambao wanafanya kazi moja nzuri sana. Nawapongeza pia kwa kuwa na mahusiano mazuri na majirani zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya Waheshimiwa Wabunge ambao wamezungumzia habari ya migogoro pengine inaweza ikaongezeka kwa sababu watu wengine walikuwa wanapata kipato katika maeneo yale. Naomba niwatoe hofu kwanza katika zoezi hili zima ambalo litakwenda kufanyika baada ya Azimio kupita maana yake elimu itakuwa ni endelevu katika maeneo yale inavyofanyika kwa wananchi wengine wanaokaa jirani na Mapori ya Akiba. Wananchi wale huwa wanapewa elimu ya kuwa walinzi wa maeneo yale na kuelezwa faida watakazozipata kutokana na ule Mfuko wa Ujirani Mwema ambao wenzetu wa TANAPA wanawasaidia.

Mheshimiwa Spika, mbali na kuimarisha uhifadhi pia, watakuwa na zoezi hilo lingine la kuona kwamba, wanajivunia nchi yao kwa kuwa na rasilimali ambazo zinaongeza kipato, lakini pia katika suala zima la kuvutia watalii wanapokuwa wanakuja katika maeneo yale, wananchi walioko kule watakuwa na fursa pia, za kuweza kufanya mambo mengine, ikiwa ni pamoja na kuwa na bidhaa za kiutamaduni ambazo itakuwa ni manufaa kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba, tumekuwa na zoezi ambalo limekuwepo chini ya TANAPA wamelifadhili katika kupanga mpango wa matumizi ya ardhi katika maeneo yanayozunguka mapori. Nina imani na nina uhakika katika hili ambalo linakwenda kufanyika sasa watu wale pia, watapata huduma hiyo ya kuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye yale maeneo, watapata fursa zote kama ambavyo wanapata wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ile hofu ya migogoro naomba tuiondoe kwa sababu, pia Serikali imedhamiria kuhakikisha kwamba, migogoro yote katika maeneo ya hifadhi, migogoro yote kwa wale wanaopakana na hifadhi inaondolewa. Kubwa ni kutoa elimu, pia kuwafanya wale wananchi wajitambue kwamba, zile ni rasilimali zao na ni sehemu ya ulinzi katika maeneo yale. Kwa hiyo, hayo wakiyajua yatakuwa hayana shida yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, napenda niseme jambo lingine katika wale watu wanaokaa katika maeneo yale, usalama utaongezeka. Tumekuwa wote tunajua unakwenda maeneo unasindikizwa na Polisi na uko ndani ya nchi yako. Usalama wa maeneo yale ulikuwa ni mdogo sana. Kwa hiyo, kwa kuyafanya kuwa hifadhi usalama utaimarishwa, lakini pia wananchi wenyewe watajiona wako salama ndani ya nchi yao. Ni maeneo ambayo kidogo yalikuwa na changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri nimefanya kazi Kagera na nilikuwa Muleba na Pori la Burigi linapakana katika maeneo hayo, kwa hiyo, maeneo yale hata ukienda kikazi ilikuwa unatakiwa uende na askari. Sasa unakwenda na askari mchana kwenye eneo lako, kwa hiyo, nina imani ulinzi utakwenda kuimarika. Kwa hiyo, tuwatoe hofu wananchi hasa wale waliokuwa wanafaidika na mapori haya. Nia ya Serikali na dhamira ni njema sana ni kuwawezesha pia wao kiuchumi katika kufungua fursa zingine ambazo zitawafanya wao pia waweze kufaidika na rasilimali iliyoko katika nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Mheshimiwa Waziri pamoja na Manaibu Waziri nawapongeza kwa kazi nzuri mnayoifanya. Nashukuru kwa miradi inayoendelea kujengwa Airport ya Mwanza, ujenzi wa jumba la wasafiri ufanyike haraka kuondoa adha ya wasafiri iliyopo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, usafiri wa ndege Dodoma – Mwanza ni vyema ukaanza kutokana na ukweli usiofichika kuwa Kanda ya Ziwa ina abiria wengi sana wanaotumia usafiri wa anga. Nashukuru nimeona fedha imetengwa kwa ajili ya fidia kwa wananchi wanaotakiwa kuondolewa eneo la viwanja. Ombi langu ni kwamba zoezi lisichukue muda mrefu ili kuondoa kero iliyopo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nimeona fedha kidogo zimetengwa katika baadhi ya barabara. Ombi langu ni kwamba barabara ya Nyakato Veta – Igombe TX kilomita 18 ina miaka mitatu; inajengwa kila mwaka kilomita moja. Naomba angalau ikamilishwe ili kuondoa mgongamano. Aidha, barabara ya Airport – Kayenze – Nyanguge Kilomita 45 ijengwe kwa kiwango cha lami ili kurahisisha wasafiri wanaoshuka uwanja wa ndege waendao Musoma waweze kutumia barabara hii badala ya kupita mjini ambako msongamano unakuwa mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa kivuko cha Kayenze – Baze unaendelea vizuri isipokuwa wasiwasi wangu ujenzi wa maegesho ya kivuko bado hawajaanza kujenga. Naomba angalau kivuko kinapokamilika kujengwa kiende sambamba na ujenzi na ukamilishaji wa maegesho hayo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi alitembelea Jimboni na kujionea adha kubwa ya wananchi wa Kigala Kata ya Buswelu kuwa na korongo kubwa ambalo limekuwa mto, limekosa daraja na tayari watoto walishachukuliwa na maji eneo hilo. Naomba ujenzi wa daraja hilo ufanyike.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mawasiliano alitembelea Jimboni tukampeleka maeneo yenye kero ya mawasiliano, hakuna mawasiliano kabisa. Orodha ya maeneo tayari nilishakabidhi. Naomba utekelezaji ufanyike ili kuondoa adha ya mawasiliano. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
NAIBU WAZIRI ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami nichangie hoja hii ambayo iko mezani ya Wizara ya Kilimo, na nianze kwa kuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa na machache ambayo yanakwenda kusaidia katika hatua ambayo Serikali inajaribu kuchukua katika kuhakikisha kwamba katika uboreshaji wa kilimo na namna ambavyo tunawezesha Wakulima wetu kuweza kupata ardhi ya kutosha na kuweza kuzalisha kama ambavyo wengi wanasema kilimo kinachukua karibu zaidi asilimia 65 kwa maana ya wanaohusika na kilimo hicho.

Mheshimiwa Spika, nianze tu kwa kusema kwamba nia na dhamira njema ya Serikali katika kuhakikisha kwamba tunakipa kipaumbele kilimo, tumeanza na ile hatua ya kuanza kunyang’anya yale mashamba ambayo yametelekezwa ili baadaye yaweze kupangiwa matumizi mazuri katika kilimo kama ambavyo Serikali imekusudia.

Mheshimiwa Spika, tuna mashamba zaidi ya 45 ambayo yamebatilishwa na mashamba haya ambayo tayari yamebatilishwa baadhi yake yameshapangiwa pia shughuli hiyo tukianza na shamba namba 217/1-6 la Mkulazi ambalo limetengwa kwa ajili ya kilimo cha miwa. Pia tunalo shamba lingine la Makurunge Bagamoyo namba 3561/1 nalo limetengwa kwa ajili ya kilimo cha miwa.

Mheshimiwa Spika, pia hatukuwaacha nyuma wananchi wetu ambao nao pia wamekuwa na tatizo kubwa katika suala zima la ardhi. Wote ni mashahidi kwamba katika Mkoa wa Morogoro nadhani unaongoza katika migogoro ya ardhi ambayo sehemu kubwa ni masuala ya maeneo ya kilimo. Kule nako katika yale mashamba yaliyofutwa tumefuta shamba namba 32, 33, 34, 35, mpaka 36, yaliyoko
Mvumi pamoja na mashamba namba 4, 5, 8 na 10 yaliyoko Msowelo lakini, mashamba haya yamerejeshwa kwa wananchi ili waendelee na kilimo kwa sababu lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba tunazalisha kwa wingi. Tunapozungumzia Tanzania ya Viwanda pia tuweze kupata malighafi itakayokwenda katika viwanda hivyo. Haya yanafanyika ili kuweza kuona ni jinsi gani tunaweza tukapeleka nguvu zaidi katika kilimo.

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi maelekezo ya Serikali pia yalishatoka kwenda katika Halmashauri zetu zote, waliombwa kutenga maeneo kwa ajili ya kilimo na hasa kwa ajili ya vijana ambayo yangeweza kutumika kwa kilimo na masuala mengine, lakini mpaka dakika hii ninapoongea ni Halmashauri chache ambazo zimeweza kuzingatia hilo. Hili lingeweza kusaidia zaidi katika kuwawezesha vijana, lakini pia kuwaweka katika maeneo hayo wangeweza kulima kilimo chenye tija. Kwa sababu wengi tunaotegemea mbali na graduates ambao wanamaliza, lakini pia hata wale walioko katika maeneo yetu ya Halmashauri, wengi wamekuwa wakiwezeshwa na Wizara husika, Wizara ya Kazi, ambayo imekuwa pia ikisaidia katika kuhakikisha kwamba vijana wengi wanapewa elimu kwa ajili ya kilimo, kwa ajili ya ufugaji na mambo kama hayo.

Mheshimiwa Spika, niziombe pia Halmashauri zetu, zizingatie maelekezo ya Serikali yanapotolewa, kwa sababu lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunainua kilimo. Kilimo kina mambo mengi ndani yake, kama hujawatambua wakulima wako kama ambavyo mtoa hoja amesema, utashindwa pia kujua wanahitaji pembejeo kiasi gani, utashindwa kujua mkwamo wao uko wapi, lakini utashindwa kujua pia, scale ya kilimo ambacho wao wanafanya, wanafanya kilimo cha biashara, wanafanya kilimo cha chakula au wanafanya kilimo gani. Ukishawatambua maana yake ni kwamba pia utakuwa unawatolea huduma kwa hao Maafisa Ugani tunaowazungumza, tunaweza kujua Afisa Ugani mmoja anahudumia wakulima wangapi? Sasa kama usipojua idadi ya wakulima, obvious hata kujua idadi ya Maafisa Ugani wanaotakiwa inaweza ikawa ngumu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kikubwa hoja ya Serikali ya kuanza kuwasajili wakulima inasaidia pia katika kuwatambua na kujua mahitaji yao ya ardhi ni kiasi, lakini pia katika suala zima la kuona kwamba tunaongeza ardhi ya kilimo, tunao wawekezaji ambao tunasema ni wawekezaji kama ambao wameshindwa, ambao wametelekeza mashamba yao, wako zaidi ya mia moja, lakini wengi wao pia wamekopea mashamba hayo. Wamekopea mashamba lakini wameenda kuendeleza maeneo mengine.

Sasa Serikali pia inapitia hawa wote kuweza kujua ni wangapi na wako wapi ili tuweze kuwanyang’anya yale mashamba yaweze kufanya kazi ile iliyokusudiwa halafu wao watafute dhamana nyingine ya kuweza kuweka katika mikopo yao.

Mheshimiwa Spika, hayo yote yanafanyika katika dhamira njema ya kuhakikisha kwamba Sekta hii ya Kilimo inaimarishwa na inakuwa pia ni chachu katika mwelekeo wa Serikali wa Tanzania ya Viwanda ili tuweze kuwa na maeneo ya uzalishaji yalio mengi na yanayozalisha kwa tija.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja. Pili, niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya. Wamebadili sana hali ya utendaji kwa watumishi waliokuwa wanafanya kazi kwa mazoea.

Mheshimiwa Spika, haja yangu, Mheshimiwa Waziri naomba kufahamu mpango wa Wizara juu ya eneo la mafunzo kwa vijana wanaosoma Chuo cha Ngozi, Mwanza. Kiwanda cha Ngozi ambacho kilikuwa kinachukua wanafunzi na kuwapa mafunzo katika Kiwanda cha Ngozi maarufu kama Mwana Tanneries. Niombe kiwanda hiki kifufuliwe upya, mwekezaji apatikane ili tuongeze ajira kwa vijana wetu.

Mheshimiwa Spika, pili, nimepokea malalamiko toka kwa wananchi wakilalamikia wafanyabiashara toka nje ya nchi wanaingia moja kwa moja viwandani na maeneo ya uvuvi ili kununua bidhaa ya samaki badala ya kununua katika soko la Mwaloni, soko ambalo liko rasmi kwa biashara ya mazao ya samaki katika Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Spika, tatu, niombe Idara ya Uvuvi wafike Jimboni kutoa elimu ya ufugaji samaki wa vizimba, ukizingatia kuwa zaidi ya 80% ya eneo katika Jimbo ni eneo la maji. Naomba tutumie maeneo ya fukwe za ziwa ambayo hayatumiki kama beach yatumike kufanya ufugaji wa vizimba (cape fishing).

Mheshimiwa Spika, nne, tunao vijana katika vikundi vya ufugaji walipata mafunzo ya awali ya ufugaji kuku, sungura na kadhalika. Niombe Wizara iwezeshe katika kuwapa mtaji ikiwemo vitendea kazi na namna bora ya ujenzi wa mabanda ya sungura, kuku na kadhalika yenye kuzingatia viwango vinavyokubalika.

Mheshimiwa Spika, tano, kuna Chama cha Ushirika cha Wavuvi ambao wameshajiunga wanasubiri uzinduzi rasmi. Niombe Mheshimiwa Waziri awazindulie ili kufungua milango kwa wafanyabiashara wengine wa samaki na wafugaji pia.

Mheshimiwa Spika, sita, ombi maalum; naomba vifaa vya uvuvi ili kuwezesha vijana waliopo katika sekta hii ya uvuvi wavue kwa tija.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mungu kwa fursa ambayo nimeipata kuweza kuchangia katika Bunge lako lakini pia kwa sababu muda ni mfupi niwashukuru sana wachangiaji ambao wamechangia kwenye Wizara yetu ni takriban Wabunge tisa ambao wamechangia. Hoja kubwa ilikuwa ni suala la kupima ardhi yote ya Tanzania kama ambavyo waliomba, lakini pia wakasema wigo wa ukusanyaji wa mapato nao bado hautoshelezi. La tatu likawa ni katika kupanga miji kama ambavyo inaonekana tulivyoanza katika ile Magometi Quarter, Wilaya ya Kinondoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane kweli na Wabunge jinsi walivyosema mpaka sasa ni takriban asilimia 25 tu ya ardhi yote nchini ambayo imepimwa. Kwa hiyo asilimia 75 yote inaonekana haijapimwa na mpaka sasa tulichoweza kupima ni viwanja 2,349,626, mashamba 28,312 na kutoa hati 1,559,509, ukiangalia kwa watu wachache kama hao bado ni tatizo kweli. Mkakati tulionao kama Wizara tumeona tutatumia approach moja ambayo inasema fit for purpose ambayo imetumika katika maeneo mengine na imeweza kuleta tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo tunachofanya sasa ni kuwajengea uwezo wataalam wetu tulionao. Tunao wataalam wachache, tunatakiwa kuwa na wataalam 2,500 kwa nchi nzima, lakini tulionao mpaka sasa ni 1,400. Kwa hiyo 1,400 hawawezi kukidhi haja katika suala zima la upangaji, upimaji na kumilikisha, lakini tunasema tutajengea uwezo wapima wakati ambao tutakuwa tunawaita para surveyors, watajengewa uwezo ili waweze kusaidia katika hili jambo la upimaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tutatumia vyuo vyetu tulivyonavyo; Chuo cha Morogoro pamoja na Chuo cha Tabora katika suala zima la upimaji. Tumejaribu katika kipindi kilichopita kutumia makampuni kwenye zoezi la upimaji shirikishi, lakini kati ya makampuni 134 tuliyoya–engage ni makampuni 34 tu ambayo yamefanya vizuri. Makampuni mengine yote yameshindwa na mikataba tumewanyang’anya. Sasa tunachofanya ni kuelekeza kwa sababu tayari mikoa yote ina ofisi na ina wataalam wa kutosha waweze kuunga nguvu katika mikoa yao jinsi walivyo kupitia ofisi za halmashauri zote, tumeshatambua wale watumishi tulionao kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kama ni suala la kupima, kupanga na kumilikisha tutalifanya kama operesheni maalum kwamba wataungana ngazi ya mkoa kwa sababu mikoa yote ina vifaa na kuna baadhi ya wilaya zina vifaa. Kwa hiyo tunaunda timu ndani ya mkoa mmoja, wanaanza wilaya moja baada ya nyingine. Kwa hiyo katika hili tumeomba pia ushirikiano wa ma-RAS pale kuweza kuongeza nguvu katika suala zima la kuunda timu kwenda katika wilaya moja baada ya nyingine. Kwa kutumia approach hiyo itakwenda kusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika suala zima hilo la kupanga makazi kama tulivyofanya Magomeni Quarter ambayo aliomba Mheshimiwa Mtemvu wa Dar es Salaam linawezekana kwa sababu pia wenzetu wa Morocco, Ethiopia wamefanya hivyo. Ni ule utayari tu wa halmashauri zenyewe kuweza kuwashawishi wananchi katika yale maeneo yakaondolewa yale makazi ambayo si mazuri ambayo ni ya kawaida sana wakajengewa makazi mengine kama ilivyo Magomeni Quarters, halafu wale wanakuwa wa kwanza kupewa kipaumbele kuweza kumiliki maeneo yale ambayo yatakuwa yamejengwa na sehemu nyingine kama ni Halmashauri zinaweza zikatumia kwa kazi nyingine. Kwa hiyo hii pia itatusaidia kuondoa adha ya majengo au nyumba zingine ambazo ziko mjini lakini hazifanani na miji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala zima la ukusanyaji wa maduhuli kama hamjapima, hamuwezi kukusanya, lakini bado tuna madeni mengi ambayo tunadai na tumeweza kusambaza notice na sasa tutasimamia sheria kwa ukaribu zaidi. Ukishapewa notice ndani ya siku 14 unatakiwa upelekwe kwenye Baraza, ukishindwa basi tunanadi vitu vyako na kama umepewa notice miezi sita kinachofuata ni kunyang’anywa ule umiliki bila kupewa taarifa, kwa sababu tayari utakuwa ulishapewa notice. Kwa hiyo hilo litatusaidia pia katika watu. Pia wale ambao wenye viwanja ambavyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, kengele imeshagonga ahsante sana.

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja.

Waliopimiwa viwanja lakini hawataki kumiliki mwaka jana tulibadili sheria hapa, Kifungu Na. 33 (1) kilibadilishwa kwa hiyo hata kama hauna hati, sisi tunaanza kutoza kodi kwa sababu tulishakupa grace period ya siku 90 uweze kuomba kumilikishwa. Sasa kama hujamilikishwa maana yake tutaanza kutoza kodi katika viwanja vyote na tumeshaanza, uwe una hati au huna hati utakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo rai yangu ni…

MWENYEKITI: Mheshimiwa, ahsante sana. Shukrani.

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: … wananchi kushirikiana na Halmashauri zote. Na tunatambua namna ambavyo TAMISEMI wameanza na sisi vile vile tunatumia watendaji wa mitaa kuweza kuwatambua wadeni wetu kuweza kukusanya kodi na kuweza kuangalia namna bora ya kupata takwimu sahihi zitakazotuwezesha pia kuweza kupata mapato ya nchi. Ahsante. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO NA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii nami kuchangia Mpango huu wa Maendeleo ambao ulikuwa unajadiliwa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru kwa Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia katika suala zima la Wizara ya Ardhi kwenye Mpango; ni Wabunge watatu ambao wamechangia. Ninachotaka tu kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge ni kwamba Wizara, inatambua wazi ya kwamba ardhi ni mali, ardhi ni mtaji, ukiitunza itakutunza.

Mheshimiwa Spika, vile vile katika suala zima la Mpango wa Maendeleo ambapo pia tunasema Tanzania inakwenda kwenye Sekta ya Viwanda na zaidi, tuko tayari; na ukiangalia kwenye ule Mpango kipengele cha 5.4.23 tumeainisha yale yote tunayokwenda kufanya.

Mheshimiwa Spika, tumeweka kipaumbele zaidi katika kupanga, kupima na kumilikisha, kwa sababu usipoipanga ardhi vizuri, utakuwa umekwamisha sekta nyingine zote katika suala zima la kimaendeleo, nasi tunatambua kwamba ardhi inahitaji kupangwa, kupimwa na kumilikishwa. Ni wazi mpaka sasa hivi hatujafikia asilimia kubwa, ni kama alimia 25 tu. Waheshimniwa Wabunge wameongelea hapa kwamba, ikiweza kupangwa vizuri na ikapangiwa matumizi, ni wazi inaweza ikakusanya kodi nyingi za kutosha. Ni kweli hatukatai hilo, lakini kama Wizara ndiyo maana mnaona kwamba Ofisi za kimikoa zilifunguliwa.

Mheshimiwa Spika, kuna Mbunge amependekeza suala la agency, ni wazo zuri, lakini kama tutatumia vizuri ofisi zile za Mikoa na Halmashauri ambazo ndiyo Mamlaka za Upangaji Miji zikaweza kukijikita katika kuweka mpango mzuri kama ambavyo upo kwenye suala zima la kutenga bajeti za kupima maeneo yao, hatutahitaji suala agency kwa sababu kila Halmashauri inao wataalam. Kila Halmashauri ikiweka kipaumbele, itaweza. Kama Wizara, katika siku za nyuma tumetoa baadhi ya pesa katika Halmashauri na wamefanya vizuri katika upangaji.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia suala la Mbeya, Kahama, Bariadi na Ilemela, walipewa fedha na wamefanya kazi hiyo nzuri. Kwa hiyo, tuna Imani, mbali na bajeti zinazokuwa zimewekwa na Halmashauri zenyewe, lakini wakiwezeshwa kidogo na Wizara, tunawasukuma kuweza kufanya kazi yao vizuri. Kwa hiyo, kama Wizara, tunaliona hilo na tunalizingatia.

Mjheshimiwa Spika, kuna suala lingine ambalo limeongelewa kuhusu kuwa na Sera ya Nyumba pamoja na Sera ya Makazi. Kama Wizara, tuko katika mchakato na tutaleta nakala kwa Wabunge ili muweze kuongeza input, kwa sababu tayari ile rasimu ya mwanzo imeandaliwa ambayo tunahitaji sasa tupate input za Waheshimiwa Wabunge kwa undani zaidi ili tuweze kutoka na final product itakayoweza kukidhi mahitaji na tutaondokana na haya malalamiko ambayo mara nyingi yanatokea.

Mheshimiwa Spika hata ile ya Real Estate Regulatory Authority nayo pia iko kwenye mchakato mzuri. Tumekuwa na madalali wengi hapa katikati na unakuta watu wengi wanadhulumiwa ardhi. Unaambiwa kuna ardhi ya uwekezaji hapa, lakini anayekwambia ni Middlemen mwisho wa siku unajikuta huwezi tena kupata ile ardhi. Kwa hiyo, sheria hiyo nayo iko ambayo, inaandaliwa kwa maana ya kwamba tutajikuta tumetoka katika suala zima la matapeli ambao wanakuwepo.

Mheshimiwa Spika, katika suala zima la uwekezaji kwenye maeneo ya viwanda ambayo hasa ndiyo tunafikiria kupeleka nguvu kule, tumetenga zaidi ya ekari 12,400 ambazo ziko tayari zinasubiri wawekezaji wakati wowote wakizihitaji. Kama Wizara pia, bado tunaendelea kupitia yale mashamba ambayo yameshindikana katika kuendelezwa ili tuweze kuyachukua na kuyatenga kwa ajili ya kazi hizo kubwa ambazo tunazitegemea kama Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa vyovyote vile, ukiweka mpango mzuri kwenye matumizi ya ardhi, ukiweka mpango mzuri katika suala zima la kupanga, kupima na kumilikisha, hizi sekta nyingine zote zitakuwa katika hali nzuri katika utendaji. Nasi kama Wizara tunasema, Serikali ilishaelekeza nini cha kufanya, kwa hiyo, Wizara tumejipanga kuhakikisha kila mpango ambao unapangwa, uwe unawiana na Wizara nyingine katika utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, hata haya ambayo yanaongelewa katika suala la kuwezeshwa kwenye maeneo ya huduma, bila kuwa na mpango mzuri na bila kufanya maandalizi, hatuwezi kufika huko. Kwa hiyo, niseme tu kwamba sisi kama Wizara, tuko tayari kuhakikisha kwamba mpango huu unatekelezeka kwa kuwa unakutekeleza yale ambayo tumeyaweka kama kipaumbele katika kuhakikisha kwamba tunakwenda kufanya.

Mheshimiwa Spika, pia katika upangaji wa miji yetu, kwa sababu usipoipanga miji pia, napo itakuwa ni shida. Kama Wizara, tayari tumeshaandaa mwongozo ambao sasa kuna mbunge alielekeza kwamba tunaweza pia tukadai kodi katika maeneo ambayo hayajapimwa. Kisheria huwezi kudai katika maeneo hayo, lakini tunaweka mpango mzuri ambao draft yake iko tayari ili zile Halmashauri katika ile miji inayokua kwa kasi, tuwape mwongozo wa namna ya kuwekeza, namna ya kupanga miji yao ili iweze kuwa na maeneo ya huduma, maeneo ya uwekezaji na maeneo ya makazi ili kila mji utakapokuwa unakua ukitangaza kama ni eneo la huduma, liwe limepangwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia katika Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuwapongeza kwa kazi nzuri ambayo wameifanya na Wabunge wote ni mashahidi wameweza kuwapongeza. Nami nawapongeza kwa kazi kubwa waliyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mazungumzo na uchangiaji wa Wabunge, kuna maeneo mawili mazuri na ni maeneo ya kimkakati kwa Taifa letu lakini Wabunge wengi hawakuyazungumzia sana, wamezungumzia masuala ya REA pamoja na vinasaba. Nataka nizungumzie maeneo mawili ya bomba la mafuta kutoka Hoima mpaka Chongoleani pamoja na Bwawa la Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Spika, nianze na Bwawa la Mwalimu Nyerere. Kama unavyotambua, maeneo mengi tunapokuwa na miradi ya kimkakati usipofanya maandalizi ya awali migogoro ya ardhi inakuwa ni mingi. Napenda nilithibitishie Bunge hili kwamba katika Bwawa la Mwalimu Nyerere, pamoja na kazi zinazoendelea, Wizara pia imehakikisha inafanya kile inachotakiwa kufanya ili kuhakikisha kwamba tunalinda maeneo yale ya vyanzo vya maji, misitu na maeneo oevu.

Mheshimiwa Spika, kilichofanyika pale ni kuwaondoa wale waliokuwepo, kulikuwa na mahoteli kama matatu; Serena Luxury, Amara Camp pamoja na Retreat Safari Ltd. Hoteli hizi zimelipwa zaidi ya Sh.3,754,000,000 ili kupisha maeneo yale. Kazi inayoendelea pale ni kupanga matumizi kwenye Mji wa Mloka pamoja na Mji wa Kisasi.

Katika Mji wa Mloka urasimishaji utafanyika kwenye kaya kama 1,000 na katika ule Mji wa Kisasi michoro 19 yenye viwanja 4,043 imeandaliwa. Kwa maana hiyo tayari tutakuwa tumeweka mazingira mazuri ili mradi unapoendelea basi kusiwepo na changamoto au migogoro ya ardhi katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini upande wa bomba la mafuta, tayari eneo la Mkuza kutoka Hoima mpaka Chongoleani utambuzi wa maeneo yale ya Mkuza umeshafanyika na kuweza kujua kama kuna maeneo yanahitaji kulipwa fidia ni maeneo kiasi gani. Tayari maeneo 12 yametambuliwa katika eneo lile ambayo hasa yataanza na masuala mazima ya ujenzi wa kambi zile ambazo zitatumiwa na wale wajenzi wa bomba la mafuta.

Mheshimiwa Spika, lakini pia katika maeneo ambayo wananchi watakuwepo pale kunapangwa miji ambayo itarahisisha kusogeza huduma za jamii katika maeneo yale kwa sababu bomba lile la mafuta litakapopita ni wazi shughuli za kijamii zitakuwepo. Kwa hiyo, tayari Sh.20,457,965,000 zitalipwa kama fidia katika yale maeneo ambapo camp hizo zitajengwa. Katika maeneo hayo watakaonufaika kwa fidia hiyo kwenye ujenzi wapo watu wa Misenyi, Kiteto, Kondoa, Iramba, Nzega, Igunga, Bukombe, Chato, Muheza, Handeni na Kilindi. Tayari utambuzi umefanyika na kinachofuata sasa ni namna ya kuweza kuona ni jinsi gani hatua hizo zitafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumechukua hatua hiyo kama Wizara ili kwanza kuleta usalama kwenye lile bomba la mafuta kwa sababu usipofanya hatua hizo za kupanga matumizi kwenye eneo lile ndiyo mwanzo sasa wa kugombania pale, watu watakuwa wana-struggle kutaka kuongezeka pale. Wizara inashirikiana na Wizara ya Nishati kuhakikisha mpango mzuri unawekwa pale ili watu waweze kukaa kwa amani kwa sababu tayari pia ni fursa kwao kwa shughuli za kimaendeleo. Maana ile miji ikipangwa tayari na uwekezaji katika maeneo yale utakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hilo nilitaka nilithibitishie tu Bunge kwa sababu wengi hawakuchangia maeneo hayo, nikaona basi kama Wizara tuseme kile ambacho Serikali imefanya kuhakikisha hii miradi mikubwa ya kimkakati inalindwa ili kuepusha migogoro na wananchi. Pia usalama wa maeneo yale tunaweka maandalizi kuweza kujua ni jinsi gani ambavyo tunaweza kufanya.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo pia kuna maeneo mengine 12 ya vituo vya kupozea, tayari wafidiwa 392 wametambuliwa. Jumla ya fidia yao ni shilingi 1,600,000,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali tayari imeshafanya maandalizi yake na tunaendelea kuhakikisha kwamba kila kilichopangwa kwenye eneo lile kinafanyika vizuri. Tumefanya hivyo ili bomba linapojengwa basi pasiwepo tena na sintofahamu katika suala zima la umiliki wa maeneo, lakini pia na kuyapanga yaonekane kwamba yamekaa vizuri.

Mheshimiwa Spika, nilitaka kuchangia hilo ili kutoa taarifa kwa Bunge lako nini ambacho kimefanyika katika hii miradi ya kimkakati. Vivyo hivyo hii inafanyika pia kwenye ile miradi ya SGR, nako Wizara ya Ardhi tupo kuhakikisha kwamba tunaepusha changamoto zinazoweza kujitokeza kutokana na matumizi ya ardhi au kwa watumia ardhi.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema, aidha, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa Rais mwenye maono na anayewapenda na kuwajali watu wake. Kazi nzuri iliyofanyika katika kuondoa kero ya maji sehemu mbalimbali ni jambo la kujivunia kama Watanzania tukizingatia kuwa maji na uhai.

Mheshimiwa Spika, mbali na sekta ya maji Mheshimiwa Rais amefanya maajabu katika sekta zote za miundombinu, elimu, afya, ardhi, kilimo na kadhalika. Mwenyezi Mungu amjalie afya njema na aendelee kulitumikia Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, ninampongeza sana Waziri wa Maji yeye binafsi, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara kwa kazi nzuri ya kumtua mama ndoo, mwenyezi Mungu awajalie afya njema muendelee kulitumikia Taifa letu.

Pili, ninakushukuru sana kwa kuweka katika bajeti Mradi wa Kabangaja wa chanzo kipya cha maji utaondoa adha ya maji Manispaa ya Ilemela.

Mheshimiwa Spika, ombi langu, wakati tunasubiri kukamilika kwa mradi mkubwa wa chanzo cha maji cha Butimba, naomba sana kupatiwa visima virefu angalau kumi tu kwa kata zilizoko pembezoni (peri urban) mwa mji ambazo hazina maji ya bomba kabisa wanatumia visima visivyo rasmi, itapendeza nao wakapata maji ya visima. Maeneo husika ni eneo la Kata za Nsumba, Kiseke; Lutongo, Kayenze; Lugeye, Sangabuye; Ilekako, Bugogwa; Isanzu, Bugogwa; Bulyanghulu, Shibula; Ibaya, Shibula; Wiluhya, Kahama; Magaka, Kahama; na Nkoronto, Bugugwa.

Mheshimiwa Spika, naomba sana Wizara ione namna ya kuwasaidia wananchi wa Ilemela ambao ziwa liko hatua chache kutoka makazi yao lakini hawana maji.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha na ninaunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa fursa hii kuchangia hoja ya Wizara ya Kilimo. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anaisimamia Wizara hii na niwapongeze Waziri pamoja na timu yake kwa kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu ni Wizara wezeshi na katika suala zima la utambuzi wa maeneo kwa ajili ya kilimo na shughuli zingine, Tume ya Mipango ya Ardhi ndio kazi yake. Ni jukumu lao kwanza la shughuli katika tume kuhakikisha kwamba wanaratibu na kuwezesha mpango wa matumizi ya ardhi yaweze kufanyika katika maeneo na kwa kipindi kifupi katika kutambua maeneo kwa ajili ya kilimo toka Mheshimiwa Rais alipowekeza na kujikita kwenye kilimo. Jumla ya hekta ambazo zimeshatambuliwa mpaka sasa ni 2,160,076. Zimetengwa kwa ajili ya kilimo kutoka katika vijiji 1,059, kati ya vijiji 2,765 ambavyo vimewekewa mpango wa matumizi. Mheshimiwa Josephine Genzabuke alizungumzia habari ya kuwawezesha wakulima na ndio hasa dhamira njema ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapowapimia wakulima maeneo yao maana yake kwanza tunaongeza thamani ya ile ardhi yao. Inapoongezwa thamani kwa kupewa ile hati, tunamwezesha pia kuondokana na migogoro, lakini tunampa uwezo wa kuitumia ile haki kwa ajili ya shughuli za kimaendeleo. Mpaka sasa tunavyozungumza jumla ya hati 1,318 zimetumika, zile hati miliki za kimila zimetumika katika mabenki kutoka kwenye halmashauri 10 katika mabenki ambayo yametoa jumla ya bilioni 60, milioni 164 zimetolewa kama mkopo kutokana na hizi hati miliki za kimila.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa maana nyingine Mheshimiwa Genzabuke alivyoliongelea, Serikali inaliangalia hili na tunajua wakulima wako zaidi ya asilimia 65 kwa sensa ya 2022. Kwa maana hiyo ni kwamba unapowekeza kwenye kilimo lazima pia umwangalie mkulima na kumwangalia kwake ni kuhakikisha kwamba ile salama ya miliki yake inakuwepo na ndio maana tunakazania katika suala zima la kuweka mpango wa matumizi ya ardhi katika maeneo, ili kila kipande cha ardhi kipangiwe matumizi. Once ukishakipangia jukumu lingine linakuwa ni la kukitumia.

Mheshimiwa Spika, wenzetu wa kilimo nawapongeza sana kwa sababu katika haya maeneo ambayo tumeyaainisha wanalo jukumu la kupima ule udongo kuona unafaa kwa kilimo gani. Kuna Mbunge mmoja amechangia akawa anasema tuwe tunaangalia na udongo unafaa kwa namna gani ili katika mazao tuangalie kikanda. Nadhani hili Wizara wameshalichukua na wanalifanyia kazi. Sisi kama Wizara ya Ardhi jukumu letu ni kuhakikisha maeneo yale yanapangiwa mpango, yanatengwa kwa ajili ya kilimo ili wao waangalie udongo uko namna gani. unafaa kwa kilimo kipi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze pia Mheshimiwa Rais katika hii program ambayo wanaendelea nayo ya BBT kwa vijana, lakini hili hajalianza leo, tuangalie pia hata kipindi kilichopita, Ofisi ya Waziri Mkuu imekwenda katika halmashauri 117 kati ya halmashauri 184, ikifundisha vijana na wamefundishwa vijana zaidi 12,000 kwa ajili ya kilimo cha kitalu nyumba. Kwa sababu tunatambua vijana wako mjini na vijijini na si wote watakaoweza kwenda vijijini kwa ajili ya kilimo ambacho kinakwenda kufanyika sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndio maana wanawekeza pia, Serikali inawekeza kwenye kilimo cha kitalu nyumba kwa maana ya ile Green House. Sasa hawa vijana 12,000 na zaidi ambao wameshapatiwa mafunzo hayo ni jukumu letu katika halmashauri zetu kuhakikisha kwamba ujuzi ule wanaulea, walioko mjini wakaendeleza kilimo, wanaweza wakafanya kilimo cha horticulture, wakati wenzao wanaendelea huku katika vijiji na maeneo mengine, maana yake hawa huku tayari wanao na wanaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka kusema kwamba, Serikali inaangalia kwa uhakika namna ya kutumia vizuri ardhi yetu na kutambua na kwa kupima na kwa kuweka mpango madhubuti. Jukumu letu sasa kama halmashauri kama Wizara huko tuliko, tuone namna bora ya kuhakikisha mpango wa matumizi kwa wenye mamlaka za upangaji, tunaipa kipaumbele sekta ya kilimo ambayo ndio sekta inayochukua zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania wamewekeza kule. Kwa hiyo hili tutalifanya kwa sababu tunajua ni jukumu letu kama Serikali kuwezesha Watanzania…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii kuchangia katika Azimio hili hasa la Kurekebisha Mpaka katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha. Nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye baada ya kuingia tu madarakani jambo la kwanza lilikuwa ni kupitia ile migogoro 975, mmojawapo ukiwa ni huu wa Hifadhi ya Ruaha na alielekeza Kamati ya Mawaziri Nane kutumia busara na hekima katika utatuzi wa migogoro hiyo. Pia akatuasa tusilete taharuki katika suala nzima hili. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, niwashukuru Wabunge ambao walianza kwa kuleta hoja hizi ambazo zilikwenda kuzaa hiyo Kamati ya Mawaziri Nane. Vilevile niishukuru Kamati, kwanza kwa kuunga mkono Azimio la Serikali lililoletwa hapa kwa sababu Kamati pia imeunga mkono na wachangiaji wengi walikuwa wanaunga mkono. Kwa hiyo, nawashukuru pia kwa kuliona hilo.

Mheshimiwa Spika, katika hoja za Kamati ambazo zimeletwa pamoja na wajumbe waliochangia nitajikita katika chache ambazo nataka kuzitolea ufafanuzi ambazo wameulizia. Jambo la kwanza ni suala la fidia ambayo wamelizungumzia. Nataka tu niseme ya kwamba kazi ya fidia mpaka sasa hivi imeshafikia karibu asilimia 80, watu wameshafikiwa kwa ajili ya kuweza kutathminiwa maeneo yao watakaokwenda kulipwa.

Mheshimiwa Spika, malipo watakayokwenda kulipwa ni pamoja na posho ya makazi ambayo watapewa posho ya pango la nyumba kwa miezi 36, kwa maana ya kufika kipindi kile atakachokuwa anaandaa makazi mengine aweze kupata pesa za kupanga, lakini atalipwa posho ya usumbufu, atalipwa posho ya usafiri atalipwa thamani ya ardhi yake pamoja na thamani ya nyumba. Haya yote yanafanyiwa tathmini na tayari asilimia zaidi ya 80 wameshafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwatoe hofu tu Waheshimiwa Wabunge walikuwa wamesema kazi hii ikamilike haraka, nadhani tunaenda nayo vizuri. Vile vile, jambo lingine ni suala zima la ule mpaka, baada sasa ya kubadilisha mipaka ya GN 28, zoezi la kuweka zile beacon katika mpaka limekamilika. Beacon zaidi 671 zimewekwa katika mpaka wa urefu wa kilometa 344, lakini na mkuza pia ambao wamesema uwekwe, mpaka sasa umewekwa kwa kilometa 177. Haujakamilika wote kwa sababu tu ya hali halisi ya hewa, kulikuwa eneo lingine lina maji hawawezi kuweka mpaka ule, kwa hiyo sasa hivi kwa sababu pameanza kukauka baadhi ya maeneo basi watamalizia. Kwa hiyo, mkuza nao umebaki asilimia kidogo kuweza kumalizia. Kwa hiyo, haya yote yanafanyika kwa sababu ni masuala ambayo ni maelekezo pia ambayo Waheshimiwa Wabunge wametoa, lakini wakaomba pia na ile suala zima la kutenganisha maeneo hayo ili yasilete mtafaruku mwingie.

Mheshimiwa Spika, katika zoezi hili zima hasa katika kuweka mpaka, wananchi kule wameshirikishwa sana kwa maana ya kwamba Uongozi wa Mkoa, Mkuu wa Mkoa Ndugu Homela alikuwa pale kwa muda wote katika suala zima hilo lakini uongozi wa wilaya pia wameshirikishwa. Kwa hiyo, mpaka huu mpya uliowekwa umeshirikisha hawa wengine. Kwa yale ambayo sasa hivi pengine Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanaona labda hayajakaa sawa sana, kama Serikali nadhani bado tunao muda wa kuweza kutafakari vizuri kuyafanyia kazi. Kwa sababu kazi hii tumeifanya kwa muda mrefu, mpaka kufikia hapa kazi imefanyika vizuri.

Mheshimiwa Spika, rai yangu ambayo naitoa tu na kuwaomba Waheshimiwa Wabunge waelewe kwamba, kazi tuliyotoa ile ya hekta zaidi ya 74,000 kwa wananchi tukienda kuifanyia mpango wa matumizi bora ya ardhi tutaweza kubaini nani anapata heka ngapi na nani atapata za kilimo na kwa maana ya wafugaji. Kwa hiyo zile hekta mpaka sasa hivi bado hazijagawiwa katika yale maeneo, kwa sababu ukikamilisha hili moja basi na mpango wa matumizi ya ardhi unaanza. Tusingeweza kufanya mpango wa matumizi ya ardhi kama hata azimio lenyewe halijapita na hatuweza kujua mipaka imefikia wapi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitoe rai tu kwamba, tupitishe azimio hili ii twende kule tuwapange wananchi vizuri, wale wafugaji ambao wameachiwa eneo la Ruaha kule waweze kupangwa vizuri, lakini na wananchi hawa ambao wanatakiwa pia kupangwa katika yale maeneo yaliyoachiwa, kwa sababu katika kuondoka ni jumla ya vijiji vitano ambavyo vinatakiwa kuondoka katika yale maeneo lakini kuna vitongoji kama kumi na kitu ambavyo navyo vinatakiwa kuondoka. Sasa wale wote tunawapangia mahali pa Kwenda.

Mheshimiwa Spika, katika hili pia tayari tumeshabainisha vijiji kumi na mbili ambako watakwenda kule lakini pamoja na hayo watapewa ile gharama ya usafiri kwa kule wanapokwenda kwa mujibu wa kisheria. Kwa hiyo, tunasema hakuna mwananchi ambaye hatatendewa haki katika hili, kwa sababu tunajua walikuwa kwenye vijiji ambavyo vinatambulika kisheria, Serikali ilikuwa imevisajili. Kwa hiyo kuwaondoa kwao pale sio kwamba ni wavamizi kwa maana ya uvamizi, lakini vilitambuliwa vijiji, kwa hiyo mipaka ndio ilikuwa inaleta taharuki kutokana na ule uhifadhi. Pia, kwa sababu wote tunaona kwamba uhifadhi ni muhimu iendelee kuwepo, basi nadhani wote tutakuwa na dhamira njema ya kuweza kupitisha azimio hili ili kazi iweze kufanyika.

Mheshimiwa Spika, naomba tu niwaombe Waheshimiwa Wabunge walipitishe azimio hili wote, kwa ujumla wao kwa sababu linakwenda kuondoa changamoto kubwa ambayo imekuwepo, lakini linakwenda kuwapa nguvu za uchumi wale wananchi ambao wataondoka. Kwa sababu maeneo watakayopangiwa yatapimwa na kila mmoja atamilikishwa kwa hati yake katika lile eneo ambalo atakuwa amepangiwa. Kwa hiyo, hapo tayari kiuchumi tutakuwa tumeshawaongezea nguvu. Kwa hiyo niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba, Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ina dhamira njema na ndio maana tunaongeza kasi ya kukamilisha michakato ya maeneo yenye migogoro ili watu waweze kuishi kwa amani, watu waondokane na kukimbiakimbia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niseme tu azimio hili limekuja kwa wakati muafaka, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge waikubali. Dhamira njema ya Serikali ni kuhakikisha tunalinda hifadhi zetu, lakini vile vile hatuleti changamoto kwa wananchi kwa sababu wao ni sehemu ya ulinzi wa zile hifadhi, wakipata maeneo wakakaa vizuri maana yake pia watakuwa ni sehemu ya uhifadhi na hapatakuwa na changamoto zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono azimio. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 3) wa Mwaka 2018
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Nianze kwa kuunga mkono hoja na niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Mwanasheria Mkuu. Nitajibu baadhi ya hoja chache ambazo zimetolewa kwenye taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani.

Mheshimiwa Spika, hoja ya kwanza ilikuwa inazungumzia suala la Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kuingilia utendaji wa Mabaraza. Naomba niseme kwamba suala hili lilishaongelewa humu ndani na lilipatiwa majibu, lakini mbali na kupatiwa majibu, Waziri mwenye dhamana ya TAMISEMI alilitolea maelekezo kwa maandishi mwezi Februari. Mimi sikutegemea kama lingekuja hapa, kwa sababu baada ya maelekezo hayo, hakuna tena jambo kama lile ambalo lilijitokeza. Kwa hiyo, nawaomba tu Waheshimiwa Wabunge kwamba pale wanapotoa hoja zao na zikafanyiwa kazi wawe wanafuatailia pia kuweza kujua, kuliko kukaa linajirudiarudia suala ambalo tayari lilishapatiwa ufumbuzi na kazi zinaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spiaka, suala la pili walikuwa wanaongelea suala la uboreshaji wa Mabaraza ya Ardhi. Ni kweli Mabaraza ya Ardhi ya Kata mengi hayafanyi kazi vizuri kama yanavyokusudiwa. Tukumbuke tu pia ile Tume ya Shivji wakati inaanza, ni nini kilisababisha mpaka Mabaraza haya yaanzishwe? Lengo pia ilikuwa ni kusogeza huduma kule chini kwa wanavijiji au kwenye mitaa kule ambako wanafahamiana zaidi. Kilichokuwa kinakusudiwa pale ni kutatua migogoro hii katika namna ya ushirikishaji zaidi. Sasa tatizo ambalo limekuwa likijitokeza sana, pengine watu wale wanakuwa wamezoeana sana, wengine wanaoneana aibu na unaweza katika utendaji unakuwa hauendi vizuri.

Mheshimiwa Spika, hili kama Serikali tumeliona, kupitia Ofisi ya Msajili wa Mabaraza tunashirikiana na Halmashauri zote kwa ajili ya kuwapa mafunzo mbalimbali wapate uelewa wa kuweza kusimamia kazi hizi. Kazi hizi pia zinafanywa na Wanasheria wa Halmashauri mbalimbali. Kuna Wilaya au Mikoa ambayo tumeshafanya nayo kazi na kazi inakwenda vizuri. Kwa hiyo, niseme kwa hili pengine ni uelewa mdogo wa wale watu wanaochaguliwa.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai tu pale ambapo zinaundwa hizi Kamati kule, waangalie watu wenye uadilifu wanaoweza kufanya kazi yao vizuri, lakini wajibu pia wa Halmashauri zetu ni kuhakikisha kwamba Mabaraza yale wanaya-own ili yaweze kufanya kazi yake kulingana na taratibu. Kwa sababu yako chini ya Mkurugenzi, yanatakiwa kuwa na bajeti zao kwa Mkurugenzi, yanatakiwa pia kuwa na mwongozo, pengine hata kuwa na By-laws zinazowaelekeza hata katika utozaji wa tozo wanazotoza pale.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana unakuta wakati mwingine hawako moja kwa moja katika utaratibu unaohusika. Serikali imeliona hili na ndiyo maana tunafanyia kazi kwa karibu sana tukisaidiana na Wanasheria wa Halmashauri. Hii imefanikiwa sana katika maeneo tuliyopita ambapo tumetoa semina hizo kwa kuwaunganisha, kazi inakwenda vizuri. Kwa hiyo, niseme hilo lilishaonekana.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia usimamizi wa sekta ya ardhi, unasimamiwa na Wizara tatu tofauti. Mabaraza ya Kata, yako chini ya TAMISEMI, lakini ukija hapa Wilayani unakuta yako chini ya Wizara ya Ardhi, akienda Mahakama Kuu, yuko Sheria na Katiba. Kwa hiyo, tunajaribu ku-harmonize namna bora ya utendaji ili kuweza kuona wanafanyaje kazi zao.

Mheshimiwa Spika, pia kwenye suala la namna ya utatuzi wa kesi zao, ukija ngazi ya Wilaya kunakuwa na tatizo. Changamoto kubwa tuliyonayo ni Watendaji hawatoshelezi, ndiyo maana unakuta Mwenyekiti mmoja anakuwa anasimamia Mabaraza matatu au manne. Hiyo tumeshaiona na kama nilivyojibu swali juzi, tayari tunao 20 ambao wataajiriwa kwenda kuziba mapengo yale. Tayari pia tumetoa maelekezo ili waweze kupatikana wengine waweze kufanyiwa vetting, kila tunapopata ajira waweze kuingia ku-solve tatizo hili. Kwa sababu lengo la kuanzisha
Mabaraza yale ni kurahisisha na kumfanya yule mwananchi wa kawaida aweze kutatuliwa kesi yake mapema na katika mazingira yale yale aliyoyazoea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo wameliongelea ni haya Mabaraza kuwa na msongamano. Wamesema kwamba Mabaraza ya Wilaya yaondolewe katika Wizara ya Ardhi na kupelekwa Wizara ya Katiba. Bado hali inarudi ile ile, kwa sababu lengo la kuanzisha Mabaraza haya ilikuwa ni kuondokana na msongamano uliokuwepo kwenye Mahakama. Kwa sababu ya nature ya migogoro ile, mingi inakwenda kutatuliwa wakati mwingine kwenye site. Kwa hiyo, huwezi kukwepa ukasema kwamba Mabaraza haya yarudi huku, utarudisha tena ule mzigo ambao tulikuwa tukiupigia kelele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naunga mkono hoja. (