Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula (147 total)

MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipatia fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Moja ya chanzo cha migogoro ya ardhi hapa nchini unatokana na kwamba katika nchi yetu sasa hivi kuna umiliki wa asili ambao unatambulika kwa mujibu wa sheria kama customary right of occupancy na umiliki kwa kupitia hati ambao unajulikana kama granted right of occupancy. Changamoto imekuwa ni kwamba katika umiliki wa asili umekuwa haupewi uzito ule ambao unastahili je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba umiliki wa asili unatambuliwa, unalindwa na kuhakikisha kwamba wamiliki wa asili wanaweza kutumia hati zao zile kwa ajili ya shughuli za kiuchumi.

Swali la pili, ujenzi holela kwenye maeneo mengi hususani katika Jiji la Dar es Salaam limekuwa ni kero kubwa sana. Sasa na moja ya changamoto ni kwamba kumekuwa na hali ambayo watumishi wapimaji pamoja na watumishi Maafisa Ardhi kushiriki katika mikakati hiyo.

Je, Serikali ina mkakati gani na nakumbuka kwamba Mheshimiwa Waziri alishawahi kutoa kauli ya kuwawezesha baadhi ya Wenyeviti wa Serikali za Mitaa pamoja na Waheshimiwa Madiwani kusimamia shughuli ya Mipango Miji na kuwapa ramani ili waweze kusimamia maeneo ya umma na kuzuia uvamizi, je, utekelezaji wa jambo hili umefikia hatua gani?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, sehemu ya kwanza Mheshimiwa ameulizia swali la miliki za asili ili kuwawezesha wananchi wetu, Wizara yangu iko katika mpango kabambe ambao unaendelea katika Halmashauri zote za kuwezesha upimaji katika maeneo ambayo yapo watu waweze kupimiwa na kumilikishwa kulingana na hali halisi katika maeneo wanayoishi. Aidha katika vipao mbele vya upangaji wa miji pia, mpaka sasa Wizara yangu imeshapima Majiji matano, Manispaa 15, Miji 15 na Miji midogo 79, yote hii ni katika kuhakikisha kwamba kunakua na mipango mizuri ambayo itaepusha ujenzi holela na ukuaji holela wa Miji yetu katika maeneo ya nchi hii.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Spika, niliuliza kuhusiana na umiliki wa asili na mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba umiliki wa asili unalindwa, kuenziwa na kutumika kwa wananchi kwa ajili za maendeleo. Lakini la pili, ni kuwawezesha wananchi, Serikali ilitoa tamko kupitia Waziri kwamba Wenyeviti wa Serikali za Mitaa watawezeshwa na kupewa ramani ili waweze kusimamia maeneo yao na kuzuia uvamizi wa maeneo, hilo swali halikuweza kujibiwa.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nadhani katika kujibu nimeeleza pengine labda hakusikia vizuri, naomba niseme kwamba, suala la maeneo kulindwa kama ambavyo Mheshimiwa Waziri alielekeza tayari katika Jiji la Dar es salaam kwa kuanzia Wenyeviti wote wale wa Mitaa watawezeshwa kupewa ramani za maeneo yao, ili waweze kila mmoja kulinda eneo lake, aweze kutambua wapi ni eneo la makazi, wapi ni eneo la wazi, wapi ambapo pamepangwa kwa ajili ya kujenga ili watu waepukane na kuvamia viwanja na kufanya ujenzi usio na utaratibu.

Mheshimiwa Spika, swali lake lingine aliongelea suala la umilikishaji wa asili kwa maana ya kupata zile hati za kimila, nadhani nimeliongelea kwamba Halmshauri zinaendelea katika utaratibu huo na ndiyo maana kumekuwa na msisitizo wa kuwa na zile masjala katika maeneo yao ili pale ambapo mwananchi anakuwa amepimiwa eneo lake na tayari Kijiji kinakuwa au Mtaa unakuwa na hati yake, basi waweke pia na eneo la kuhifadhi. Maana yake huwezi kuwa na Mmliki wa Asili na kutoa hati ambazo huna namna ya kuweza kuzihifadhi, maeneo yote wameelekezwa kuwa na masjala ambazo zitatunza na tunaimani kwamba hati hizi zinawapa uwezo wananchi kiuchumi kwa hiyo suala hilo Wizara inaitilia kipaumbele ni wajibu wa Halmashauri zote kuzingatia na kufuata utaratibu huo.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu kumekuwa na migogoro katika nchi yetu baina ya wananchi na hifadhi, lakini tatizo hili limekuwa haliishi kwa Wizara hizi mbili ya Ardhi na Maliasili kukaa pamoja na kumaliza matatizo haya.

Nahitaji kufahamu kutoka kwa Serikali ni lini Wizara hizi mbili watakaa pamoja kumaliza migogoro ya Wananchi katika Vijiji ambavyo vinapakana na hifadhi mfano, Wananchi wangu wa Wilaya ya Babati na hifadhi ya Tarangire.
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gekul, Mbunge wa Babati na Mjumbe wa Kamati ya Ardhi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba iko migogoro inayosababishwa na mipaka kati ya Vijiji na Hifadhi za Misitu, Hifadhi za Wanyama na migogoro hiyo tunaijua na ni kweli kwamba hata katika maeneo anayotoka Mheshimiwa Mbunge ya Tarangire na sehemu nyingine tuliiona hiyo. Sasa tumekubaliana ndani ya Serikali katika awamu hii ni kuhakikisha kwamba aina hii ya migogoro yote tunaiondoa, na ndiyo maana nimeandika barua kuwapeni Waheshimiwa Wabunge nafikiri mtapewa leo. Nimeomba kila Mbunge aniambie aina ya migogoro iliyopo katika maeneo yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najua kama Serikali tuna utaratibu wetu wa kupata taarifa lakini nilitaka nipate taarifa za pande mbili. Iko migogoro kati ya vijiji na vijiji, iko migogoro kati ya mipaka ya vijiji na vijiji na Wilaya, iko migogoro kati ya vijiji na Hifadhi za Misitu na wanyamapori na mengine, kwa maana hiyo tukipata hizo taarifa na zile tulizoagiza Mikoani sisi kama Serikali tutakaa pamoja.

Najua hapa tunahusika, Waziri mwenzangu wa Maliasili anahusika, Waziri wa TAMISEMI anahusika tutakaa pamoja na tutaunda timu na sisi tutakwenda pamoja kuhakikisha kwamba tunaondoa migogoro hii kwa manufaa ya Wananchi wetu.
MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nashukuru sana Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Naomba niongeze maswali mawili ya ziada. Serikali iliagiza Wakurugenzi wa Halmashauri waorodheshe mashamba ambayo yametelekezwa na wameshafanya hivyo. Je, ni lini Serikali itakwenda kutupa majibu ya moja kwa moja?
Swali la pili, kwa kuwa kuna wawekezaji wana mashamba makubwa mfano mashamba ya Miombo Estate, Kilosa Estate, SUMAGRO, Isanga Estate ambao wamebadilisha matumizi na kuvunja sheria na utaratibu, Je, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu wa kuyarudisha mashamba hayo kwa wananchi wa Jimbo la Mikumi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli maelekezo yalikwishatolewa kwa Wakurugenzi wote na hasa kupitia katika Ofisi za Wakuu wa Mikoa ili kuweza kuainisha migogoro yote iliyopo katika maeneo hayo ili Wizara iweze kuchukua hatua mpaka sasa mashamba ambayo tayari yamekwishaainishwa na kuletwa pale Wizarani ni jumla ya mashamba 75, lakini pia tunavyo viwanja 694. Haya yameainishwa ni katika mashamba yale kuanzia mwaka 2002 mpaka 2015 na utoaji wake sasa tayari uko katika process za kawaida.
Mheshimiwa Spika, vile vile kwa wale ambao wameshindwa kabisa kuendeleza na tayari mapendekezo yameshaanza kushughulikiwa kwa ajili ya kubatilishwa kwa mujibu wa kifungu cha 48 cha Sheria ya Ardhi, Sura ya 113 tunatarajia pia kuwa kazi hiyo itafanyika kwa mujibu wa sheria na kanuni, kwa sababu haya yako katika utaratibu na maelekezo yamekwishatolewa.
Waheshimiwa Wabunge, ninachowaomba kwa sababu pia kila Mbunge alipata maelekezo hayo ambayo tunawaomba mfanye kazi hiyo kwa kusaidiana na Halmashauri zenu muweze kuleta na kuainisha migogoro yote na siyo migogoro yote inapaswa kuletwa Wizarani kuna mingine ambayo pia inaweza ikamalizwa na ofisi zetu za Kanda kwa sababu tuna ofisi karibu katika Kanda nane nchi nzima. Kwa hiyo, kuna mengine yanaweza yakatatuliwa katika maeneo hayo ilimradi tu taratibu nilizozitaja katika jibu la msingi basi ziweze kufuatwa na Wizara itakuwa tayari kuyashungulikia.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa Wilaya ya Arumeru Mashariki kwa kiasi kikubwa ardhi yake inamilikiwa na wawekezaji na ni ukweli mara nyingi kumetokea migogoro kutokana na wananchi kuwa na mahitaji makubwa ya ardhi, na kwa kuwa mpaka sasa mnasema ni ekari 80 tu imerudi katika Halmashauri ya Wilaya ya Arumeru, je, Serikali haioni sasa uko umuhimu wa kupitia mashamba hayo na kufanya tathmini upya ili wananchi hawa ambao wanahitaji ardhi waweze kupata ardhi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Mkoa mzima wa Arusha maeneo mengi pia ardhi yao imemilikiwa na wawekezaji ikiwemo Wilaya ya Karatu ninayotoka na kumekuwa na mgogoro mkubwa sana wa wananchi kuhitaji ardhi kwa sababu ardhi nyingi imemilikiwa na wawekezaji mfano Shamba la Tembo Tembo liloko Karatu. Je, Serikali sasa iko tayari kufika Wilaya ya Karatu na kufanya tathmini ya kuwatambua wawekezaji ili wananchi waweze kupata ardhi yao?
NAIBU WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ametaka kujua Serikali ina mpango gani katika kuyatambua mashamba yote haya na kufanya tathmini ili yaweze kugawiwa kwa wananchi. Naomba niseme kwamba mpaka sasa Waziri alishapeleka barua katika Mikoa yote ikiwataka kwanza wao wayatambue kwa sababu wanayafahamu, lakini mpaka sasa Wizara yangu imeshabaini mashamba 22 katika Mkoa wa Arusha ambayo tayari yameshabatilishwa kwa minajili ya kuja kuwagawia wananchi wenye shida ya maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili anazungumzia habari ya mgogoro na uhitaji wa ardhi katika eneo la Karatu. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mimi mwenyewe nilifika Karatu na migogoro hiyo niliambiwa na wakati huo nilikuwa nashughulikia masuala ya Mabaraza ya Ardhi. Hata hivyo, kwa sababu Wizara imeweka mpango mzuri kwa ajili ya kuweza kuyafikia maeneo yote kwa wakati, tunajaribu kukusanya migogoro yote na ndiyo maana tuliomba tuweze kuipata na tuko tayari kurudi tena Karatu kwa ajili ya kutatua mgogoro huo ambao anauzungumzia. Kabla ya Bajeti ya Wizara kuisha, Wabunge wote watakuwa wamegawiwa vitabu na wataweza kubaini migogoro ambayo tumeiainisha ambayo tunatarajia kuanza kuitembelea baada ya Bunge hili kumalizika. Kwa sababu migogoro ya ardhi ni suala mtambuka na Wizara zingine zitahusika. Kwa hiyo, kila Mbunge ataona katika Mkoa au Wilaya yake ni migogoro ipi ambayo Wizara imeiainisha kwa ajili ya kuipatia ufumbuzi.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na yenye maana. Mwaka jana mwezi wa Sita niliomba Serikali iende mpaka Korogwe ikaangalie maeneo ambayo hayaendelezwi na Serikali iliniahidi kwamba ingekwenda kule na kukagua mashamba ambayo hayaendelezwi ili ufanywe utafiti wa kuwagawia wananchi, hadi leo hii na mimi nilienda kwenye mikutano ya hadhara na kuwaambia wananchi kwamba Naibu Waziri atakuja kuangalia mashamba ambayo hayaendelezwi na watu wakakipa sana kura Chama cha Mapinduzi kwa kujua kwamba viongozi wanafika.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kushangaza mpaka leo hii hawajafika na badala yake nasikitika sana baadhi ya Watumishi wa Halmashauri wanaleta habari ambazo siyo njema, zisizoweza kumsaidia mtu wa aina yeyote. Naomba Waziri, ni lini mimi na wewe tutakwenda mpaka Korogwe Vijijini ukaone huku kudanganywa kwamba ni shamba moja katika mashamba 17 yanayozunguka Jimbo langu hayajapatiwa ufumbuzi.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niseme kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwa kupitia swali la Mheshimiwa Ngonyani.
Mheshimiwa Naibu Spika, ikiwa kama kila Mbunge atataka Waziri afike kwenye eneo lake na kufanya utambuzi wa mashamba zoezi la ukaguzi wa mashamba haya yasiyoendelezwa halitafikia ukomo. Hata hivyo, najua wazi kwamba ni jukumu la Halmashauri zetu husika ambapo na Wabunge ni Wajumbe kuweza kuyatambua hayo mashamba na Wizara inapofika pale, inakuja baada ya kuwa imepata taarifa ili kujihakikishia kwamba kilicholetwa ni sahihi, tutafika pia kukagua, lakini hatuwezi kufanya ile kazi ya mwanzo, unakwenda kila eneo kukagua halafu ndiyo uweze kuchukua hatua, maana utashindwa kuchukua maamuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima Halmashauri husika ilete mapendekezo halafu Mheshimiwa Waziri apeleke kwa Mheshimiwa Rais kwa ajili ya ubatilisho. Maamuzi ya matumizi yanafanyika ndani ya Halmashauri kwa sababu ndiyo wenye mamlaka pia ya kugawa mashamba hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe tu Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu zoezi hili Mheshimiwa Waziri alishalitolea maelekezo na alitoa barua katika maeneo yote, ni jukumu letu sasa kuanza kukagua yale mashamba tuliyonayo ambayo Halmashauri zetu imeyatoa. Hivyo, Wizara inarahisisha kazi baada ya kuwa imeshapata kutoka kwenu, sisi tutakuja kutambua ili sheria zisikiukwe na kuleta malalamiko kwa Wizara.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Mheshimiwa Ngonyani iwapo itabidi, basi tutafika, lakini kazi hii ni kazi ya Halmashauri.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri maswali mawili ya nyongeza. Imekuwa ni jambo la kawaida kwa Serikali kuwaacha wananchi mpaka wamejenga na baadaye Serikali utakuta inachukuwa hatua sasa ya kubomoa nyumba za wananchi ambao tayari wamekaa pale kwa muda mrefu.
Je, haionekani kwamba sasa inaweza kupelekea matatizo kwa wananchi na kushindwa kujiweza na kujimudu kutafuta makazi mengine? (Makofi)
Swali la pili; je, ni lini sasa Serikali itasimamia Mipango Miji yake kama sheria inavyotaka kama ambavyo amekuwa akizungumza Mheshimiwa Waziri ili kuondoa tatizo hili?
Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza naomba kujibu kwamba, siyo kweli kwamba tunawaacha wananchi wanaendelea na kazi za kujenga bila kuwazuia. Tatizo lililoko ni katika Halmashauri zetu ambazo mara nyingi katika kutoa katazo mtu anapokuwa amekiuka wanaweka pengine alama ya X, lakini wakati huo huo pia wanaendelea na shughuli za maeneo mengine pasipo kufuatilia kwa karibu.
Mheshimiwa Spika, kwa hatua hiyo, Wizara kama Wizara, sasa hivi imechukua hatua na tumeanza na Mkoa wa Dar es Salaam. Tunapeleka usimamizi kwa viongozi wa maeneo hayo na ndiyo maana tumetoa pengine Ramani kwa Wenyeviti wa Mitaa ili aweze kutambua maeneo yake na mpango uliopo katika yale maeneo ili kuweza kujua lipi ni eneo la wazi, lipi ni eneo ambalo halitakiwi kujengwa?
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuna imani kwamba kama watatoa ushirikiano watakuwa ni sehemu ya usimamizi na hapatakuwa na mwananchi yeyote ambaye atakuwa amejenga kinyume cha sheria kwa sababu usimamizi tayari utakuwa chini ya viongozi wa maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, swali la pili nadhani limejibiwa pamoja na la kwanza kwamba ni lini tutafanya hivyo? Tayari hatua tumeshazianza. Natoa rai tu kwa sasa kupitia Bunge hili kwamba, tuombe Halmashauri zetu, kwa sababu maeneo mengi ambayo watu wanajenga kiholela; wapo wanaoona, wapo ambao wanakaa kimya na hawafuatilii.
Tuombe tu sasa kwamba popote pale ambapo mtu atajenga kinyume na utaratibu, halafu na uongozi wa pale upo unamwona mpaka anamaliza, atakapovunjiwa nyumba yake, kiongozi husika wa eneo lile atawajibishwa ikiwa ni pamoja na kulipa fidia kwa yule ambaye amekiuka taratibu na yeye akiwa anashuhudia.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante, kwanza kabisa nimpongeze Waziri Lukuvi na timu yake kwa kunifungulia Baraza hili la Ardhi na hata watu wa Wilaya ya Lushoto sasa walimuombea dua maalum Lukuvi na timu yake kwamba kama kuna gagaziko basi liondolewe Mungu awaletee wepesi liweze kuondoka. Sasa naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza;
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Waziri amekuja kutufungulia Baraza la Ardhi lakini bado tuna migogoro mikubwa ya ardhi kati ya kijiji cha Nywelo na msitu wa Shume; kati ya Shamba la Mkonge Mnazi na vijiji vya Kwemng‟ongo na kijiji cha Kwemkwazu; kijiji cha Kwetango na kijiji cha Kweulasi; kijiji cha Kwemashai na kijiji cha Kilangwi.
Je, ni lini Serikali itakuja kutatua migogoro hiyo?
Swali la pili; Kwa kuwa, Wilaya ya Lushoto yenye Tarafa za Lushoto, Mlola, Mlalo, Mtae, Umba, Bumbuli, Soni na Mgwashi. Je, ni lini sasa Serikali itapima maeneo yao kwa kuwapatia hati za kimila ili wapate fursa za kukopa kwenye mabenki kuinua uchumi wao?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na hilo la mgogoro wa ardhi kati ya Mkonge Mnazi Estate na vijiji vya Kwemkwazu na Kwemhong‟o, Kwemlazi na Kwetango, Kwemashai na Kilangwi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, unajua haya majina ya watani wangu kidogo ni magumu kutamka usipoangalia unaweza ukakosea, lakini nadhani nimeyataja vizuri. Kwa sababu tulikwishatoa maelekezo na kwenye kitabu cha migogoro, mgogoro huu umetajwa na hatua za kuanza kwenda kutatua au kutwaa tena lile eneo kuna hatua za kupitia ikiwemo na kutoa notes kwa mhusika, tayari Halmashauri wamekwishatoa notes kwa huyu Mmiliki wa Mnazi Estate, kwa hiyo mara muda wa notes zile siku 90 zitakapokuwa zimekwisha, basi hatua zingine zitachukuliwa ili kuweza kumaliza kabisa mgogoro huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana ndugu zangu, watani zangu wa Kwemashai, Kilangwi, Kwaulasi, Kwetango na Kwemkwizu na Kwemng‟ongo kwamba notes zikikamilika hatua kamili zitachukuliwa kama atakuwa ameshindwa kujitetea kama tunavyotarajia.
Swali lake la pili ameulizia habari ya upimaji katika Tarafa za Lushoto, Mlalo, Mlola, Mtae, Umba, Bumbuli, Soni na Mgwashi. Naomba tu nimhakikishie kwamba iwapo tutapitisha pia bajeti ambayo ndiyo inakwenda kupitishwa leo, tayari kule tumetenga pesa kwa ajili ya upimaji, takribani bilioni 8.8 ambazo zinakwenda kununua vifaa na vifaa hivi vitagawiwa katika ofisi zetu za Kanda ili watu waweze kupima katika maeneo kwenye Kanda zao ikiwemo haya maeneo ya Lushoto, Mlalo, Mtae, Umba, Bumbuli na maeneo mengine kama nilivyotaja hizi Tarafa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye suala la umilikishaji ardhi ambapo tunataka watu wote wawe na umiliki halali kwa maana ya kuwa na hati, tayari katika bajeti yetu tumetenga bilioni 13.8 ambazo zinakwenda kufanya kazi ya umilikishaji wa ardhi. Kwa hiyo haya yote yatakwenda kufanyika mara bajeti yetu itakapokuwa imepita, pia ni jukumu la Halmashauri zetu kuwa tayari katika suala hilo kwa sababu suala la upimaji pamoja na kwamba Wizara inafanya kazi hii, pia Halmashauri zinapaswa kujipanga vizuri kuweza kuona ni namna gani wanafanya matumizi bora ya ardhi katika baadhi ya vijiji vyao. Kwa sababu kiasi hiki bado kinaweza kisikidhi upimaji katika maeneo yote. Hivyo, kila Halmashauri inakumbushwa pia waone nao ni jukumu lao pamoja na kwamba Wizara itafanya kazi hiyo kupitia hizi pesa zilizotengwa, lakini bado Halmashauri wanao wajibu wa kupima maeneo yao.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika nashukuru kwa kunipatia nafasi hii.
Kwa kuwa Wilaya ya Mkalama ni miongoni mwa Wilaya mpya ambazo hazina Mahakama ya Ardhi na huduma hiyo inapatikana Kiomboi.
Je, ni lini Wizara itaona umuhimu wa kutupatia Mahakama ya Ardhi na kuteua Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza katika majibu ya swali la msingi, lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba tunasogeza huduma hizi kwa wananchi kwa kufungua Mabaraza mengi kama ambavyo tumeyataja namna ambavyo nilisema kwamba tayari Mabaraza 47 Gazeti la Serikali lilikwisha yatangaza. Kwa hiyo kwenye suala la kufungua Baraza la Ardhi katika Wilaya ya Mkalama, naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba pale ambapo tutakuwa tumehakikishiwa eneo kwa ajili ya Mahakama, ambapo tumeomba pia Wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya katika yale maeneo yenye uhitaji mkubwa waweze kutupa maeneo hayo ili kuweza kufanya. Hivyo, tutaweza kuangalia tukiona kama eneo lipo zuri la kuweza kutosha basi tutaweza kufanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa tuliyonayo pia, hawa Wenyeviti wa Halmashauri bado ni wachache ukilinganisha na Mabaraza tunayotaka kufungua. Kwa hiyo bado tutakuwa na Wenyeviti ambao watakuwa wanahudumia pengine zaidi ya Baraza moja kulingana na uchache wao. Pale ambapo tutapata ajira mpya basi tutaweza kuwaeneza katika maeneo yao, kwa sasa naomba tu Waheshimiwa Wabunge tuvumiliane katika hilo kwa sababu lengo ni zuri, ni jema lakini bado uhitaji ni mkubwa kwa maana ya Wenyeviti wa kuweza kufanya kazi hiyo. Pale tutakapokuwa tumewapata basi tutafanya kazi hiyo.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa kwa muda mrefu sana kumekuwepo mgogoro wa wananchi na Serikali kwa maana ya Hifadhi za Serikali na wananchi wamekuwa wakilalamika sana kwa sababu watu wameongezeka lakini ardhi haiongezeki:-
Je, ni lini sasa Serikali italeta sheria Bungeni ili ifanyiwe marekebisho kuweza kumaliza mgogoro baina ya wananchi na Serikali?
Swali la pili, kwa kuwa kuna mgogoro mkubwa na wa muda mrefu katika Hifadhi ya Pori la Kagerankanda na Serikali; na wananchi wamekuwa wakipata shida sana kutokana na shida iliyopo kwa sababu kwa muda mrefu hifadhi haijafanyiwa marekebisho ya kupimwa mipaka:-
Je, ni lini sasa Mheshimiwa Waziri tutafuatana kuja Kasulu kwa ajili ya kumaliza suala la Mipaka katika Wilaya ya Kasulu katika eneo la Kagerankanda?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, ametaka kujua ni lini Serikali italeta sheria ambayo itakwenda kumaliza migogoro kati ya Serikali na Wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme tu, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, mgogoro uliopo pengine unaweza kuwa umchangiwa pia na baadhi ya watumishi wetu, kwa sababu 2002 mhifadhi aliyekuwa katika ile mbuga alikwenda akabainisha mipaka ambayo ilikosewa, matokeo yake ikabidi warudie tena 2009 baada ya mhifadhi mwingine kubadilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mhifadhi alipobadilisha tena naye mgogoro ukawa mkubwa zaidi. Ndiyo maana hapa sasa Serikali ilibidi iingilie kati katika kuangalia ile GN iliyokuwepo na kuweza kujua mipaka halisi ni ipi. Kwa sababu mgogoro umekuwa mkubwa zaidi, ndiyo maana pia Mkuu wa Wilaya ya Wanging‟ombe akaunda Tume kwa ajili ya kutaka kutatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimelizungumza hili la mipaka kwamba lina matatizo, tutakwenda kushirikiana Wizara zinazohusika kwa sababu huu mgogoro hauhitaji kutungiwa Sheria, ni namna tu ya kutafsiri mipaka katika eneo ambalo lina mgogoro. Wananchi wanadai wako nje, lakini mipaka ya hifadhi, wahifadhi wanasema wako ndani ya hifadhi. Ndiyo maana nimesema, hapa tutakaa Wizara yangu ya Ardhi, Wizara ya TAMISEMI pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalalii ili tumalize huo mgogoro.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ameongelea pori la Kagerankanda; nalo lina mgogoro na wananchi na akataka tuongozane kwenda Kasulu kwa ajili ya utatuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, baada ya kikao hiki cha Bunge na baada ya kukutana Wizara zote zinazohusika na migogoro hiyo kama ambavyo imewasilishwa na Waheshimiwa wabunge na siyo huu mgogoro wa Kasulu tu na migogoro mingine, tutapanga ratiba maalum ya kufika katika maeneo ili tuweze kutatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika sasa ni kujua chanzo cha mgogoro: Je, ni Wizara inatakiwa kwenda na Wizara nyingine au uko kwenye mipaka kwa maana ya TAMISEMI au ni hifadhi pamoja na ardhi ili tuweze kujua?
Mheshimiwa Naibu Spika, tukishabainisha kwa sababu orodha tunayo kwa Majimbo yote au kwa nchi nzima, basi tutatatua kulingana na nature ya mgogoro wenyewe.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa Wilaya ya Mpanda Manispaa nusu ya eneo lake halina ramani kabisa hususan Semulwa, Kichangani, Makanyagio kuelekea Misunkumilo pamoja na majengo ya katikati ya mji; na kwa kuwa, Serikali inasema sasa TRA itachukua kodi kila eneo na hawa wananchi hawana hati wala uhakika wa eneo lao kwa sababu mpaka sasa hivi hakuna upimaji wa aina yoyote na Wilaya ya Mpanda ni Wilaya Kongwe, je, Serikali itapima lini maeneo hayo ili wananchi sasa watambue haki yao ili waweze kupata mikopo kutoka kwenye benki zetu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa Wilaya ya Mpanda Manispaa Mabwana Ardhi wanachukua mashamba ya wananchi na kugawa viwanja lakini wale wananchi hawawapi viwanja. Je, ni lini Serikali au ni lini tutaenda na Naibu Waziri akajihakikishie hali ilivyokuwa korofi ya migogoro ya ardhi ndani ya Manispaa ya Mpanda?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nianze na ufafanuzi wa swali lako. Tunapoongelea maeneo ambayo yako demarcated ni kwamba upimaji wake ulishafanyika kwa maana ya michoro kamili lakini bado haujatenga maeneo kukamilisha upimaji kujua kiwanja kipi kinaishia wapi. Kwa hiyo, ni maeneo ambayo tayari michoro na viwanja vipo lakini bado havijawekewa mipaka yake na kuweza kukamilika kama inavyostahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza la Mheshimiwa Lupembe ameeleza kwamba karibu nusu ya eneo katika wilaya hiyo bado halijapimwa na ametaja baadhi ya maeneo kama Changani, Kanyageni, Sukuma na majengo ya katikati ya mji na kwamba Wizara inasisitiza habari ya kuchukua kodi, je, ni lini tutapima? Katika jibu la msingi nimesema kwamba tayari kama Wizara tumeshagundua hayo na tumeona matatizo jinsi yalivyo na jinsi ambavyo watu wanakosa haki yao ya msingi ya kuweza kuwa na ule umiliki halali wa ardhi na kuwa na hati zao ambazo zingeweza kuwasaidia pia kufanya shughuli nyingine za maendeleo ikiwa pia ni pamoja na kujipatia fursa za kupata mikopo benki. Ndiyo maana tumetangaza zabuni na tukataka Halmashauri zote ambazo wana hayo maeneo ambayo upimaji wake haujakamilika kufanya upimaji ili tuweze kuwa na uhakika wa maeneo na watu waweze kumilikishwa ili tunapochukua kodi, basi tuchukue ile kodi ambayo ni halali na iko katika maeneo sahihi ambayo tayari yako katika utaratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni Halmashauri nyingi ambazo bado hazijakamilisha upimaji. Ndani ya Wizara tuna viwanja zaidi ya 240,258 ambavyo tayari upimaji wake upo lakini haujakamilika na Kanda ya Mashariki inaongoza kwa kuwa na viwanja karibu 102,000. Kwa hiyo, tunasema kwamba, ukamilishaji huu umetangaziwa zabuni ili uweze kukamilika na tuweze kumilikisha watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili anasema, baadhi ya Maafisa Ardhi wanachukua mashamba na kupima viwanja halafu wenye mashamba hayo hawapewi stahiki zao kwa maana ya pengine ya kupewa viwanja. Naomba nirudie tena kulisema hili, tulilizungumza pia wakati tunahitimisha bajeti ya Wizara, tulishasema ni marufuku kuchukua mashamba ya watu pasipo kukamilisha fidia zao. Kwa sababu unapotaka kupanua mji, tunajua ni miji mingi ambayo imeiva katika kupimwa sasa kuwa miji halali lakini tunawataka sana wananchi wasiwe rahisi sana katika kutoa mashamba yao kwa sababu wanapunjwa sana na Halmashauri zote hazitakiwi kuchukua mashamba ya watu pasipo kukamilisha taratibu za ulipaji fidia katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwambie tu Mheshimiwa Lupembe hakuna Afisa Ardhi yeyote anayeruhusiwa kuchukua ardhi ya mtu bila kumpa stahiki zake. Hata kama limeiva katika upimaji, basi taratibu zile za fidia zifanyike ndipo Halmashauri iweze kuchukua eneo hilo.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwanza nianze kwa kuishukuru Wizara ya Ardhi kwa kazi nzuri wanayoifanya. Kwa kuupendelea Mkoa wa Tanga, Wizara ya Ardhi ilitoa shilingi milioni 50 kwa ajili ya kuangalia mashamba ambayo hayaendelezwi lakini fedha ziko mikononi mwa mtu na Korogwe hawajafika na hawajafanya utafiti wowote na badala yake wanakwenda pale kwa ajili ya kumdanganya danganya tu Waziri wa Ardhi. Je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari twende wote mpaka Korogwe tukaangalie yale maeneo ambayo hawajapewa wananchi na yameachwa kama misitu ili atusaidie kutatua tatizo la wananchi wa Korogwe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Profesa Maji Marefu ambaye ni mtani wangu, amekuwa akifuatilia sana suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spka, ni kweli katika utoaji wa pesa kwa ajili ya kubaini mashamba ambayo pengine hayajaendelezwa ili tuweze kuyatwaa, Korogwe walipewa shilingi milioni 50 kwa ajili ya kazi hiyo. Cha kusikitisha ni kwamba, pamoja na pesa ile kupelekwa lakini kazi iliyokusudiwa ni kama haijafanyika kama tulivyotarajia. Hata Waziri alipokwenda alipewa taarifa za maeneo mengine na haya mashamba yaliyoko Korogwe taarifa ile haukutolewa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niseme kupitia Bunge lako hili, Wizara inapotoa pesa kwa nia njema ya kutaka kumaliza migogoro ya watu iliyoko katika maeneo hayo, tunaomba sana wale Maafisa wanaopokea hizo pesa wawatendee haki wananchi ambao wamekuwa na kero ya namna hiyo. Kwa hiyo, kwa suala la kutaka kwenda kujiridhisha katika hilo na kwa sababu Wizara ilishapeleka pesa, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Stephen Ngonyani kwamba tutakuwa tayari kwenda kufuatilia suala hilo ili tuweze kujua zile shilingi milioni 50 zimetumikaje ili hatua za kinidhamu ziweze kuchukuliwa ikiwa kama kulikuwa na ufujaji wa pesa.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa kuna baadhi ya maeneo ambayo wananchi wamelipia katika eneo la Kigamboni - Kibada na wamepewa hatimiliki na nina ushahidi kamili kwa sababu mimi ni mmojawapo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ile ya Kigamboni - Kibada kuna eneo ambalo watu wamepewa hatimiliki na mpaka hivi sasa watu wameshindwa kujenga kutokana na wananchi fulani fulani wanasema ni maeneo yao na ukitaka kwenda kujenga wanaandamana. Je, Serikali inalijua hilo? Kama inalijua, italichukulia hatua gani suala kama hilo ili watu waliopewa hatimiliki waweze kujenga nyumba?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Faida Bakar kuhusiana na mgogoro ambao uko katika eneo la Kigamboni hasa katika eneo la Kibada kama alivyolitaja.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kwanza nimhakikishie kwanza, migogoro ya Kigamboni ambayo imekuwepo kwa sasa ni kama imepungua na Mheshimiwa Mbunge wa eneo lile amekuwa akifuatilia mara kwa mara kuweza kujua watu wake hatima yake inakuwaje. Kwa hiyo, nimhakikishie tu kwamba, pamoja na kwamba kuna ule mradi ambao unasimamiwa na Wizara ambao umechukua karibu hekta 6,000 katika lile eneo lakini bado kuna maeneo mengine ambayo yana migogoro kama alivyoitaja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Wizara imetoa maeneo katika eneo la Kigamboni ambapo kuna wapimaji ambao wamepima maeneo yao. Ni kweli kuna watu ambao wana hati zao na wameshindwa kuendeleza kutokana na migogoro hiyo. Kwa sababu mgogoro huu ni mkubwa, Wizara yangu itakuwa tayari kwenda kuhakiki katika maeneo yale yote ambayo watu wana hati zao lakini kila wakitaka kuendeleza kuna watu wanaandamana ili tuweze kuondoa mgogoro huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kigamboni imekuwa kama ni jicho la Wizara katika kuona kwamba ule mpangilio unaokwenda kufanyika pale unafanyika kwa taratibu ambazo ni za kisheria na ambazo zitakuwa hazikuvunja haki za wamiliki wa awali katika upande huo. Kwa hiyo, namhakikishia tu kwamba suala hili tutalifanyia kazi na tutachunguza yale yote ambayo yanalalamikiwa katika utaratibu mzima wa umilikishaji wa ardhi.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Napenda kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali. Kwa kuwa tunataka kwenda kwenye nchi ya viwanda na tunataka kuwawezesha kimtaji wafanyabiashara na wakulima, je, Wizara ina mkakati gani wa haraka kuhakikisha kwamba mashamba ya wakulima hasa wa Mkoa wa Simiyu na Mikoa ya jirani yanapimwa na kupatiwa hati ili kusudi wakulima waweze kwenda kwenye mabenki na kukopa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Stanslaus ametaka kufahamu ni lini Wizara itapima mashamba hayo na kuwamilikisha watu ili waweze kupata hati. Naomba niseme tu kwanza suala la kuanza kupima viwanja katika maeneo ni lazima Halmashauri yenyewe husika iweze kuyatambua na kuyabaini maeneo ambayo sasa yameiva kwa ajili ya upimaji kwa sababu siyo maeneo yote ambayo yanahitaji kupimwa kwa sasa. Kwa hiyo, tunachosema ni kwamba yale ambayo yameiva na yanahitaji kupimwa na ili kweli tuweze kupata maeneo ya kuweka viwanda kama tunavyosema nchi inaelekea kwenye viwanda lazima Halmashauri ilete mashamba hayo ambayo tayari yatakuwa yamepitia katika taratibu za kawaida za kubainishwa katika Kamati zao za Mipango Miji ili tuweze kujua sasa eneo hili linahitaji kupimwa kwa ajili ya matumizi ya viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima iende sambamba na mpango kabambe wa maeneo hayo kwa sababu hatuwezi kupima tu kwenye maeneo ambayo hayana plan ambayo imekaa katika utaratibu wa mpango wa muda mrefu wa maeneo hayo. Kama haya mashamba anayoyasema tayari yako katika mpango kabambe wa Jimbo lake, basi ni vizuri tukayajua ili Wizara iweze kuchukua hatua hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama tulivyosema, tumetenga pesa shilingi bilioni 8.8 kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji na vifaa vitakwenda kila kanda. Kwa hiyo, vitakapofika Kanda ya Ziwa ni wazi na Simiyu vitafika ili kuweza kupima mashamba haya ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyataja.
MHE. SOPHIA M. SIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na nina maswali mawili ya nyongeza.
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali ni chanzo kikubwa cha migogoro ya ardhi mijini kwa kuangalia wananchi wakijenga maeneo ambayo hayaruhusiwi na wanajenga majengo makubwa, mazuri na matokeo yake Serikali inashindwa kulipa fidia kutokana na gharama kubwa. Je, Serikali itaweka utaratibu gani wa kuwapa nguvu maafisa mbalimbali wa chini
wakiwemo Wenyeviti na Watendaji wa Mitaa kuhakikisha maeneo haya hayavamiwi? (Makofi)
(b) Kwa kuwa wananchi walioamishwa Kipawa kupelekwa Kinyamwezi baadhi yao mpaka leo hawajalipwa fidia. Je, Serikali inasema nini kwa sababu imewaletea wale wananchi umaskini, inabidi wauze vile viwanja na kwa hiyo umaskini unaendelea. Naomba anihakikishie, hawa ambao wako Kinywamwezi siku nyingi, wamepelekwa hawana la kufanya, hawana pesa ya kujengea watalipwa lini sasa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza amezungumzia habari ya kupewa nguvu wananchi ili kuweza kuzuia pasiwepo na ujenzi holela kwa sababu watu wanajenga majengo katika maeneo yasiyoruhusiwa na baadaye wanabomolewa. Naomba niseme tu kwamba, nadhani ilikuwa ni Aprili kama sikukosei ambapo Wizara ilichukua hatua mahsusi ya kushirikisha Wenyeviti wa Serikali za Mitaa katika maeneo mbalimbali kwa kuwapatia ramani na tulianzia kwenye Mkoa wa Dar es Salaam. Lengo la Wizara kutoa ramani hizi kwa viongozi wa maeneo hayo ni kutaka pia kuwafanya wao wawe na wajibu wa kuweza kulinda maeneo yao. Kwanza watambue eneo lao na matumizi ya ardhi katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni wazi wakishaona ile ramani na kwa sababu walielezewa pia, kwa sababu kumpa ramani peke yake bila kufungua akili na mawazo yake na akajua maana ya michoro ile inakuwa ni kazi bure lakini walielezwa wapi pana maeneo ya wazi, wapi panastahili kujengwa nini na wapi hapastahili kujengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, lengo la Serikali kutaka kuwapa nguvu kwanza ni kuwapa yale mamlaka yao kamili kuweza kuwa sehemu ya ulinzi wa maeneo yao kuepuka ujenzi holela ambapo wakati mwingine watu wanabomolewa kwa kujenga maeneo yasiyoruhusiwa, maeneo ambayo yanahitaji pengine kuwa na jengo fupi mtu anajenga jengo refu lakini hayo yote tumewawezesha Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Kamati zao waweze kuyatambua. Napenda kusema kwamba tunatakiwa kuendelea kutoa ramani hizo kwa Wenyeviti ili kero ya Dar es Salaam isije ikaenda na maeneo mengine ili tuanze kudhibiti kabla haijafika ingawa kuna maeneno mengine pia yana tatizo hilo hilo.
Kipawa na Kinyamwezi ni lini watalipwa stahiki zao waache kusumbuliwa ili waweze kujenga nyumba zao? Nimesema kabisa kwamba, sheria iliyotumika kipindi kile cha kuwalipa ilikuwa inazungumzia suala zima la Land Acquisition Act ya mwaka 1967.
Mheshimiwa Naibu Spika, ile sheria ilikuwa inataka tu mtu alipwe kwa maendelezo yaliyopo na anapewa kiwanja ili aweze kwenda kujenga tena katika maeneo mengine. Kusema kwamba Serikali pengine itawawezesha ili waweze kujenga, hilo halitawezekana kwa sababu sheria haitaki ifanyike hivyo. Sheria ikishakupa thamani ya maendelezo yako, ikakupa na kiwanja, sasa ni jukumu la wewe kufanya hivyo. Uzuri ni kwamba thamani inayotolewa ni ile iliyoko katika soko. Kwa hiyo, tuna uhakika kwamba pengine inaweza ikamwezesha mwananchi kurudia katika hali yake.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwa kuwa wananchi wa Kipunguni Serikali inakiri kabisa kwamba haijawalipa fidia na kwa kuwa Serikali imeonyesha kabisa nia ya wazi kwamba wanalihitaji eneo la Kipunguni kwa upanuzi wa Uwanja wa Ndege, je, Serikali ina mkakati gani sasa wa muda mfupi kuwasaidia wananchi wale wa Kipunguni kwa kuwa hawana maendeleo na wala hawakopesheki?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mariam Kisangi ameuliza Serikali ina mkakati gani wa kuweza kuwawezesha wananchi hao ili waweze kuondokana na adha waliyonayo? Naomba nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kama tulivyoeleza wakati wa bajeti kwamba tunakwenda kupitia taasisi zote ambazo zinadaiwa na wananchi kwa maana wametwaa maeneo yao lakini hawajalipa fidia ili tuweze kuwasisitiza waweze kulipa fidia hizo mapema. Kwa sababu ni kweli imekuwa ni muda mrefu, hata kama utapiga hesabu kwa kuweka 6% bado inakuwa ni ngumu kwa sababu kadri wanavyochelewesha kulipa ndivyo jinsi mwananchi anavyozidi kuumia. Kwa hiyo, Wizara inachukua hatua kwanza kuwabaini wale wote ambao wanadaiwa kwa maana kwamba wametwaa maeneo ya wananchi ili waweze kuwalipa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kama hiyo haitoshi, Wizara imetoa Waraka Na. 1 wa mwaka 2015 wa Uthamini na Ulipaji wa Fidia ambao unataka kwa siku za baadaye, iwe taasisi au mtu binafsi akitaka kuchukua eneo la mtu ni lazima alipe kwanza fidia na Wizara lazima ijiridhishe kwamba kuna pesa ambayo ipo itakwenda kulipa watu hao kabla ya maeneo hayo kuchukua ili kuepuka hii migogoro ambayo imekuwa mingi. Kwa hiyo, Waraka Na.1 wa mwaka 2015 sasa hivi tunausimamia na wakati huo huo tunawafuatilia wale ambao wanadaiwa kuweza kuwa-push ili waweze kulipa fidia za watu ambao wanawadai.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa migogoro ya ardhi hapa nchini ni mingi na kwa kuwa migogoro ya ardhi inafanana, je, Serikali ina mapango gani wa kumaliza tatizo la Tabora Manispaa katika Kata ya Malolo ambalo mpaka Mheshimiwa Waziri wa Ardhi alifika akaona hali halisi na akatoa maelekezo lakini mpaka sasa halijatekelezwa? Je, kwa leo Serikali inatoa tamko gani kwa tatizo la Malolo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanne Mchemba ambaye anataka kujua ni lini Serikali itamaliza mgogoro katika Manispaa ya Tabora kama alivyolielezea. Naomba niseme kwamba, Waheshimiwa Wabunge wote ni mashahidi kwamba migogoro ya ardhi imekuwa ni mingi sana kama hivyo amekiri wazi kwamba Mheshimiwa Waziri alikwenda na akatoa maelekezo lakini bado mgogoro ule haujamalizika na hata wakati amekwenda bado kulikuwa na migogoro mingine katika maeneo hayo. Kwa hiyo, tumejikuta kama Wizara pengine unakwenda ku-solve mgogoro mmoja ukirudi unakuta mwingine uko pale pale katika lile eneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilichukue hili suala la Mheshimiwa Mchemba kwa sababu tayari maelekezo yapo. Nitakachofanya ni kufuatilia kuweza kujua kwa nini yale maelekezo ya Mheshimiwa Waziri hayakutekelezwa mpaka leo halafu tuweze kuchukua hatua kwa wale ambao walipewa maelekezo hayo. Kwa sababu kwa sehemu kubwa wale Makamishina Wasaidizi katika Kanda ambao wapo wanatakiwa pia maagizo yakishatolewa na Mheshimiwa Waziri waweze kusimamia utekelezaji wake mpaka mwisho. Kama hili halijatekelezwa, ni wazi hata Kamishna Msaidizi wa Kanda ile hajatekeleza wajibu wake kama jinsi anavyopaswa kufanya. Kwa hiyo, tutalifuatilia kuweza kujua ili hatua ziweze kuchukuliwa.
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Tatizo la ufidiaji liko pia katika Jimbo langu la Morogoro Kusini hasa kwenye Kijiji cha Kivuma. Kuna mwekezaji amekuja pale ameanza kuchimba mawe bila kulipa fidia kwa wahusika. Je, nini kauli ya Serikali kwa mwekezaji huyu ambaye hajalipa fidia kwa wahusika wenye umiliki wa ardhi wa pale Kivuma?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Omary Mgumba amesema kwamba kuna mtu ameanza kuchimba mawe katika eneo ambalo wananchi wake hawajalipwa fidia. Kwa sababu hatuhitaji kuendelea kuwa na migogoro isiyo na msingi na kama hajalipa fidia na huu ni mgogoro mpya pengine ambao umeanza siyo siku nyingi kwa sababu sina uhakika kama uko kwenye ile orodha ya migogoro, nimtake Mkurugenzi wa Halmashauri husika afike kwenye hilo eneo aweze kuangalia mgogoro uliopo na kutoa ufumbuzi wa mara moja kwa sababu ni suala ambalo linahitaji sheria ikamilike katika utekelezaji wake ndipo huyu aendelee na kazi yake ya uchimbaji. Kama hajakamilisha, basi ni lazima Mkurugenzi asimamie hilo kuhakikisha wale watu wanapata haki yao na huyu aweze kuendelea na shughuli yake.
MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Emmanuel Papian.
MHE. EMMANUEL P. JOHN: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kutokana na hali ya Kiteto ilivyo na wote mnafahamu, ningependa Mheshimiwa Waziri aniambie ni lini angeweza kufika Kiteto na kuzungukia hayo maeneo kama Waziri wa Ardhi, aweze kuona na kufanya mikutano ya hadhara ili aweze kuzungumza na wananchi wamweleze kero zao zaidi ya hapo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, naomba Wilaya ya Kiteto ipimwe maeneo yote kwa maana ya kila mtu ajue kipande chake cha ardhi ili kuepusha ile migogoro inayoendelea kwa sababu leo tunaendelea, lakini bado kuna vuguvugu la migogoro inayoendelea. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBANI NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ameuliza ni lini tutazungukia Kiteto na kufanya mikutano ya hadhara. Naomba nimhakikishie tu kwa sababu zoezi hili la migogoro utatuzi wake utafanyika kwa nchi nzima na kama ambavyo Wizara imeshatoa kitabu cha migogoro, hivyo, muda unakapowadia katika suala zima la kuanza kuzungukia maeneo hayo na Kiteto pia tutafika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameulizia ni lini sasa ardhi yote ya Kiteto itapimwa. Kama Waziri alivyotoa kwenye bajeti yake tumeanza na wilaya tatu ambazo ni wilaya za mfano ambazo tunakwenda kuanza nazo kazi na wameshaanza katika Mkoa wa Morogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la upimaji ni suala ambalo linagharimu pesa nyingi na kama tulivyoeleza wakati tunatoa maelezo wakati tunamalizia bajeti, tulisema kwamba, halmashauri pia zinapaswa kutenga pesa kiasi kidogo ili kuweza kuanza upimaji katika maeneo yake, wakati Wizara pia inajipanga katika kuhakikisha kwamba ardhi ya nchi nzima inapimwa.
MHE. SALMA M. MWASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante. Pia nashukuru kwa majibu ya Naibu Waziri lakini nina maswali mawili ya nyongeza:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kuna migogoro ambayo hasa inatokana na tatizo la usimamizi mbovu wa sera. Kwa mfano, kuna matatizo yanayotokana na hawa Viongozi wa Serikali za Mitaa kuuza maeneo ya umma kama shule, zahanati, majeshi na hiyo inatokana na kwamba Serikali haijaweka zile demarcation au kutoa hati miliki katika maeneo hayo, kwa hiyo, hicho ni chanzo cha migogoro. Je, ni lini Serikali itapima haya maeneo ya umma ili kuondoa migogoro hii hasa kwa Jiji la Dar es Salaam?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, fidia ni tatizo pia, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba wanaanzisha Mfuko wa Fidia. Kuanzisha Mfuko wa Fidia tu sio suluhu ya mgogoro. Mgogoro wa fidia unatokana hasa na yule mlipaji kutokuwa na hela stahiki wakati anafanya uthamini. Je, ni lini sasa Serikali itasimamia kabla ya schedule ya kwenda kuthaminiwa na Mthamini Mkuu wa Serikali yule mlipaji wa fidia awe tayari ameshaweka hizo hela kwenye Mfuko wa Fidia? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ameulizia suala la tatizo la watu kuvamia maeneo ya Taasisi. Hata kabla ya upimaji ambao unatakiwa kufanyika kwa nchi nzima, Wizara ilishaelekeza kwa halmashauri zote kuhakikisha kwamba, maeneo yote ya umma yaweze kupimwa na hii inafanyika katika Halmashauri zenyewe husika kwa sababu ni maeneo ambayo wako nayo na wanayatambua katika maeneo yao. Kwa hiyo, haya hayasubiri ule upimaji wa Kitaifa ambao unaendelea kwa sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotakiwa ni Halmashauri zenyewe ziweze kulinda maeneo yake na kama hiyo haitoshi, tumekwishaanza zoezi kwa Dar es Salaam ambapo Wenyeviti wa maeneo husika wamepewa ramani za maeneo yao kuweza kutambua maeneo yapi ya wazi, yapi ya umma na yapi ambayo yanatakiwa kuangaliwa ili yasiweze kuvamiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwakumbushie tu kupitia katika swali la Mheshimiwa Mwassa, halmashauri zote zihakikishe kazi ya upimaji maeneo yanayomilikiwa na Taasisi mbalimbali ifanyike ili kuepusha migogoro ambayo inaendelea kutokea siku hadi siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ameongelea suala la fidia, nadhani tulishalijibu katika hotuba wakati tunazungumzia na bado nitaendelea kulijibu tu. Ni kwamba, Mfuko wa Fidia umewekwa pale ili kuweza kukaa tayari katika kupitia yale masuala ambayo yatakuwa yana migogoro ambayo haijatatuliwa katika ukamilifu wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata h ivyo, Wizara kazi yake siyo kulipa fidia katika maeneo ambayo yanatwaliwa na Wawekezaji au na watu binafsi katika maeneo hayo. Ni jukumu lao kuona kwamba analipa fidia, Wizara imetoa maelekezo, haitaweza kupitisha uthamini wowote utakaoletwa, yale majedwali yatakayoletwa, kabla ya kujiridhisha kwamba kuna pesa ambayo imeshatengwa na ndiyo maana Mfuko huu utakuwa na bodi yake ambayo itafanya kazi zake katika kuhakikisha pia wanajiridhisha na kile ambacho Wizara imeelekeza kabla ya fidia kulipwa au kabla ya watu kuondolewa katika maeneo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishawaelekeza kama Wizara, hakuna mtu kuondolewa katika eneo lake kabla hajalipwa fidia. Kwa hiyo, hilo ni lazima lizingatiwe kwa wale wanaokuwa na mawazo ya kutwaa ardhi za watu.
MHE. ZAINAB M. VULU: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante. Namshukuru pia Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nina maswali mawili ya nyongeza:-
La kwanza, kufuatana na maelezo ya Wizara husika kwamba mashamba yasipimwe viwanja kwa ajili ya ujenzi wa nyumba. Je, hawaoni kwamba wananchi watanyimwa haki zao kwa sababu mtu anapokuwa na mashamba yake ana ndugu zake, ana watoto wake, ana wake zake atataka awagawie maeneo ya kuweza kujiendeleza na kukwepa ujengaji holela katika miji yetu, Serikali haioni kwamba itamnyima haki huyo mhusika wa hilo shamba?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kutokana na tatizo la mgogoro wa mipaka kati ya Ikwiriri na Nyamwage kwa maana ya Kata ya Mbwara na ni wa muda mrefu. Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kuutatua mgogoro huo na kuwawezesha wananchi wa Wilaya ya Rufiji kuweza kuwa na mji mdogo katika Jimbo la Rufiji? Naomba majibu na tuambiwe lini wananchi hao watatatuliwa mgogoro huo na kupewa majibu.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge kulingana na swali alilouliza kwamba mashamba yasipimwe, kutopimwa mashamba hayo kufanywa viwanja kutanyima haki ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuelewe kwamba tamko la Wizara lililotolewa ni kwa ajili ya faida na manufaa ya halmashauri zetu wenyewe kwa sababu watu wamekuwa wakitumia njia hiyo kujinufaisha katika kupima, kununua mashamba baadaye wanapima viwanja na wanaviuza katika bei kubwa sana, square meter moja inauzwa 20,000 na kuendelea na ni baadhi ya Wabunge pia wamelalamika katika hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa na wakati mwingine pia unaporuhusu hiyo, watu wanaanza kuanzisha miji ambayo haiko katika utaratibu wa mipango miji kulingana na mipango kabambe ambayo imewekwa katika maeneo hayo. Kwa hiyo, hatuwezi kuruhusu hilo liendelee, kama kazi hiyo itakuwa iko ndani ya mpango wa Halmashauri inaweza ikafanyika hivyo ,lakini suala kubwa hapa ni kwamba, halmashauri zetu zinaibiwa au Serikali inaibiwa na haipati pesa. Hakuna tatizo lolote la yeye kupeleka mpango wake halmashauri na halmashauri ikafanya kazi hiyo ya ugawaji viwanja na mapato ya Serikali yakaingia kuliko yeye kudanganya kwamba anataka shamba baadaye anapima na kupunja wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, kuhusu mgogoro wa Kijiji cha Ikwiriri na Nyamwage, samahani Mheshimiwa kama nitakuwa nimetaja vibaya. Nyamage?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Nyamwage! Naomba niseme migogoro hii iko mingi kama ambavyo tumeelekeza sasa inakuwa ngumu sana kwenda leo, kwenda Ikwiriri, kesho unarudi unaitwa tena kulekule katika eneo lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tunafanya uratibishi kama Wizara kuweza kujua migogoro yote hii ili timu inapokwenda kufanya utatuzi wa mgogoro huu wa Ikwiriri ikatatue na migogoro mingine katika maeneo hayo badala ya kwenda mgogoro mmoja baada ya mwingine ambayo inagharimu Serikali pesa nyingi ya mtu kwenda na kurudi kwa hiyo tutafanya utatuzi huu katika migogoro yote kama jinsi ambavyo tutakuwa tumeikusanya ambavyo tumeleta kitabu na bado mnaendelea ku-update taarifa zilizoko humu.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, namshuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Hata hivyo, bado watu wa Kata ya Rasbura Kijiji cha Mitwero wanaendelea kulalamikia kuhusu tatizo hili ambalo lipo. Fidia ambazo wamelipwa wananchi wale ni ndogo kiasi kwamba wanashindwa kununua maeneo mengine mbadala ili waendelee kufanya shughuli zao. Je, Serikali itawasaidiaje wananchi hawa kupata maeneo mengine mbadala ili waendelee kufanya shughuli zao?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, katika jibu langu la msingi nimesema kwamba Wizara yangu ikishirikiana pia na Ofisi ya Manispaa ya kule, kuna utaratibu uliokuwa unafanywa wa kupitia upya maeneo yale ili kuweza kuona wale ambao wamelipwa fidia ndogo kulingana na thamani ya ardhi ambayo imetwaliwa wanapata stahiki zao. Ndiyo maana nimesema zoezi hili lilikuwa linafanyika upya. Mpaka wakati huu napozungumza, baadhi ya taasisi ambazo zilikuwa zimechukua maeneo hayo zimekwishawalipa watu hao fidia zao na wanaendelea na taratibu zao za kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, suala la kusema kwamba tutawasaidiaje kupata maeneo, unapotoa ardhi yako kwa mtu au taasisi kinachotakiwa kulipwa ni ile fidia stahiki ambayo itakufanya wewe pia uweze kupata eneo lingine la kuanzisha makazi mengine au maendeleo mengine kwa kadri ambavyo utakuwa umejipanga. Kwa sababu fidia yoyote inayochukuliwa lazima iende na bei ya soko. Tatizo tulilonalo, baadhi ya wananchi wanakuwa na ule uharaka wa kutoa ardhi yao na wanapewa fidia ndogo ambayo haiwezi kuwafikisha mahali ambapo wanastahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kupitia Bunge hili tunasema kwamba ni marufuku kwa watu kuwanyanyasa wananchi kwa kuwapa fidia ndogo ambazo hazikidhi mahitaji. Ndiyo maana vilevile tumesema kuanzia sasa hakuna ardhi itakayotwaliwa bila Wizara yangu kujiridhisha na fidia ambayo itakuwa imetathminiwa kwa wale ambao ardhi yao inakwenda kutwaliwa, ni lazima fidia ifuate bei ya soko itakayokuwepo kwa wakati huo.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa tatizo la Kata ya Rasbura linafanana na tatizo lililoko Kata la Lusonga Jimbo la Mbinga Mjini ambapo Halmashauri ilitwaa eneo ambalo lilikuwa linamilikiwa na wananchi kwa malengo ya kupima viwanja na kuliboresha eneo lile lakini mpaka sasa fidia bado haijalipwa na viwanja bado vinaendelea kugawanywa kwa watu wengine. Serikali haioni sasa hiyo formula inayotumika kule Lindi ikatumike na Mbinga yaani kulirudia tena kulipima upya na wale wananchi wa Lusonga wapate haki yao?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, wazo lake ni zuri, nami nalikubali kama Wizara. Kikubwa ambacho nataka kusema ni kwamba, kabla ya utoaji wa ardhi katika maeneo yoyote, tuwaombe sana Halmashauri zinazohusika lazima wahusishe Ofisi ya Mthamini Mkuu ili waweze kuona kwamba tathmini itakayofanyika haimpunji mtu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa sababu anasema kule kwake kuna tatizo, namwomba sana, kwa sababu hatujapata kwa maandishi kwamba kuna matatizo hayo, ashirikiane na Kanda yetu ya Ardhi kule kwa maana ya Kamishna ili waweze kuliangalia suala hili. Kama kuna malalamiko ambayo yapo, basi ofisi itakuwa tayari kuyasikiliza na kuweza kuipitia upya. Kwa sababu hatujalipokea, siwezi kulitolea jibu la moja kwa moja, isipokuwa ni kushirikiana na Kamishna wa Kanda katika Kanda ambayo Mheshimiwa anatoka.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mwaka 2011/2012 Bunge hili liliazimia kuanzisha Mabaraza ya Ardhi matano. Miongoni mwa Mabaraza hayo ni pamoja na Wilaya ya Tunduru kuanzisha Baraza la Ardhi lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza Wilaya ya Tunduru katika Baraza lile la Ardhi bado halina Mwenyekiti, Mwenyekiti ni lazima atoke Songea aje Wilayani Tunduru. Ni lini sasa Serikali itachukua hatua ya kuona kuwa tunapata Mwenyekiti ambaye atakuwa anashughulikia migogoro ya ardhi iliyopo Wilayani Tunduru? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza swali lake liko nje na lile swali la msingi lakini kwa sababu ameuliza naomba tu nitolee maelezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa bajeti ya Wizara tulitoa orodha ya Halmashauri zote au Wilaya zote ambazo Mabaraza mapya yanakwenda kuanzishwa na yalikuwa ni Mabaraza 47 ambayo yamepangwa, lakini kwa kuanzia tukasema ni Mabaraza matano. Kesi yake katika Jimbo lake analolisema tunaitambua lakini kulingana na ule ufinyu wa bajeti iliyopo tumeshindwa kuwa na Wenyeviti wa kutosheleza Mabaraza hayo ambayo tutakwenda kuanzia nayo. Ndiyo maana tulisema tumeomba ombi maalumu kwenye Wizara ya Utumishi ili kutupa kibali tuweze kupata Wenyeviti tuwasambaze katika maeneo yote ambayo hayana Mabaraza na ambako kuna matatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo, pale ambapo tutapewa kibali hicho, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye Baraza analolizungumzia ambalo halina Mwenyekiti kwenye Jimbo lake basi tutampatia. Kwa sasa bado tunasubiri kibali kutoka Wizara ya Utumishi.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Miji ya Sumve, Nyamatala, Malya, Nyambiti, Hungumarwa inakua kwa kasi sana. Mheshimiwa Waziri katika ziara yake aliyoifanya Kwimba nilimuomba vitendea kazi kama gari na vifaa vya kupimia. Nataka kujua ombi letu hilo limefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nilitembelea kwenye Jimbo lake na hayo anayoyasema tuliyazungumza. Kikubwa ambacho nataka nimhakikishie, katika bajeti yetu ambayo imepitishwa na hata kwenye bajeti ya Wizara ya Fedha ambayo tunaendelea kuijadili, kuna fedha kiasi cha shilingi bilioni 8.8 zimetengwa kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji kwa sababu tatizo la upimaji ni tatizo kubwa katika nchi yetu na tunasema eneo lililopimiwa ni asilimia 15 tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pale ambapo tutakuwa tumefanikiwa kupata pesa hizo baada ya kuwa tumepitisha bajeti hii tunajua hizo shilingi bilioni 8.8 kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji ziko pale. Tukishapata, vifaa hivyo vitakwenda katika Kanda. Jimbo la Sumve liko kwenye Kanda ya Ziwa, kwa maana hiyo, eneo la Kanda wakipata vifaa hivyo basi upimaji katika maeneo ya Nyamatala na mengine aliyoyasema yatafanyiwa upimaji kwa wakati muda utakapofika.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Japokuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema majibu yatakuwa ni yaleyale na mimi naomba nikumbushie.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la Maswa linafafana na tatizo lililoko Ulanga katika Kata ya Ilagua, Lupilo, Minepa na Milola ambapo Mheshimiwa Rais aliahidi kuhalalisha hili eneo la buffer zone ili wananchi hawa wafaidi tunu ya pekee ya ardhi tuliopewa. Je, ni lini Serikali itahalalisha na itatekeleza ahadi hii ili wananchi hawa wafaidi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika,ahsante. Kwanza nimshukuru pia Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maliasili kwa majibu mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nimkumbushe Mheshimiwa Mbunge kwamba maswali haya mengi yanayohusiana na migogoro ya mipaka na hasa pale yanapogusa Wizara zaidi ya moja tulikwishayazungumzia na kuyatolea maelekezo. Kama alivyojibu Naibu Waziri wa Maliasili Wizara tutakwenda kukaa, tutafika kwenye maeneo ambayo yanahusika baada ya wataalam kuwa wamepitia maeneo hayo na kujua ile mipaka inayolalamikiwa kuona kama kweli mpaka ulipanuliwa na kufuata watu au mahitaji ya watu yamekuwa ni makubwa kiasi kwamba sasa inahitajika kuangalia upya mipaka iliyowekwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, suala hili ningeomba sana Waheshimiwa Wabunge wawe na uvumulivu kwa sababu ni maeneo mengi yana mgogoro huo na maeneo mengi yanahitaji pia kupitiwa upya ili kuweza kukidhi ile haja ambayo Waheshimiwa Wabunge wanaiona kwamba inafaa kwa wakati huo. Ahsante.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Pamoja na majibu hayo naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa masjala za ardhi ambazo zimejengwa katika Vijiji vya Nakalonji, Mbondo, Namatunu pamoja na Nahimba hizo ambazo zilikuwa zinadhaminiwa na watu wa MKURABITA. Maana ni muda mrefu toka zimeachwa mpaka sasa hivi zinataka kupotea?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili nataka nijue, ni nini mantiki ya Serikali kuanzisha Vijiji vya mfano; kwa mfano hivyo vijiji vinne ambavyo nimevitaja ambavyo jukumu hili limeachwa mikononi mwa Halmashauri wakati wanajua Halmashauri zetu hazina uwezo au hazina uchumi wa kutosha kuweza kugharamia kukamilisha hizi hati ambazo mpaka sasa hivi zimesimama na wananchi bado hawajapata?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza alitaka kujua ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa masjala kwa ajili ya kuhifadhia hizo hati miliki za kimila. Kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, kwa sasa Halmashauri inafanya juhudi za kutenga bajeti kila mwaka ili kuweza kukamilisha zoezi hilo. Siyo kujenga tu masjala pia kuna hati 1,170 kama nilivyosema ambazo ziliachwa zilikuwa hazijakamilika kutoka katika hivyo Vijiji vya Mbondo, Nakalonji pamoja na Nahimba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pale ambapo watakuwa wametenga fedha ya kutosha kuweza kukamilisha, basi zoezi hili la kujenga masjala na kukamilisha zile hati miliki za kimila ambazo ziliachwa na MKURABITA zitakamilika. Hili ni jukumu pia la Halmashauri wenyewe kuhakikisha kwamba zoezi hili linakwisha, kwa sababu lilikuwa limeshaanza vizuri lakini baadaye likaishia katikati.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili anasema nini mantiki ya kuanzishwa vijiji vya mfano katika hili. Mheshimiwa Mbunge labda naomba tu tuelewane kwamba zoezi hili linapofanyika lengo lake kubwa pia ni kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa na maeneo ambayo yapo kiusalama zaidi. Usalama wenyewe ni pale ambapo unakuwa tayari umeshapimiwa eneo lako vizuri, unayo hati yako ya kimila ya kumiliki, hapo tayari unakuwa na uhakika wa eneo lile kuwa nalo salama. Taasisi hizi ambazo pengine zilikuwa zikisaidia zilishindwa kukamilisha malengo hayo na kuona kama vile mradi ule haukuwa mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia mradi huu ulikumbana na changamoto za ukosefu wa fedha. Lengo la Serikali ni kuhakikisha tunakuwa na Miji iliyo salama lakini miji ambayo pia imepangika. Kikubwa zaidi ni kumwezesha yule mwananchi kumiliki hati yake ya kimila ambayo itamsaidia, hawezi tu kuwa nayo kama hana pia mahali pa kuhifadhia, haya yote yanakwenda katika utaratibu huo wa pamoja.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba lengo la Serikali kuanzisha Vijiji vya mfano ni la msingi na zuri, tunaendelea nalo na ndiyo maana sasa tunazitaka Halmashauri ambazo zilikuwa na huo mradi katika ile miradi ambayo haikwisha, basi waendelee kuweka pesa kidogo kidogo wakamilishe ili kuweza kufikia ile azma ya Serikali ya kuwa na usalama wa milki kwa watu wetu.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii ili niweze kuuliza swali la nyongeza kwa niaba ya wananchi wangu wa Mji wa Tunduma. Swali la kwanza; Mji wa Tunduma ni mji uliopo mpakani mwa Tanzania na Zambia na ni lango kuu la nchi za Kusini na Kati mwa Afrika. Kwa tafsiri hiyo ni kwamba wageni wote kabla hawajingia katika nchi ya Tanzania ni lazima wapitie Tunduma kutoka katika nchi hizo.
Je, Serikali ina mpango gani wa makusudi na wa haraka wa kupima ardhi katika Mji wa Tunduma ili kuondoa ujenzi holela unaoendelea kwa hivi sasa? (Makofi)
Swali la pili; nini mwongozo wa Wizara ya Ardhi ikishirikiana na TAMISEMI kupitia Halmashauri zetu kwenye Idara ya Ardhi ili kutoa fursa kwa Halmashauri kukopa fedha katika taasisi za fedha, lakini pia kukubali makampuni binafsi ambayo yanaweza yakapima ardhi mfano UTT katika maeneo yetu ili kuhakikisha kwamba tunapunguza ujenzi holela katika maeneo yetu ya Mji wa Tunduma na maeneo yote nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza, nikubaliane naye kwamba ni kweli Tunduma ni lango kuu na lipo mpakani na uingiaji wa watu pale ni mkubwa sana kwa hiyo panahitaji kuwa na mipango iliyo thabiti. Ameuliza tuna mpango gani wa kupima ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, jukumu la kupima ardhi siyo la Wizara peke yake, Halmashauri zenyewe zinatakiwa kuwa na mipango yake ambayo inakuwa imeandaliwa. Wizara inakwenda kutoa msaada hasa wa wapimaji labda na vifaa kupitia Kanda pale ambapo Halmashauri imeshindwa yenyewe kutekeleza jukumu hilo. Kama mna mpango huo tayari Tunduma, Wizara yangu itakuwa tayari kushirikiana nanyi kuhakikisha kwamba maeneo yale yanapimwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ametaka kujua nini mwongozo wa Wizara katika suala zima la upimaji kwa kutumia mashirika au makampuni binafsi ukatolea mfano wa UTT. Naomba niseme tu kwamba, Wizara tayari imeshabainisha makampuni 55 na orodha kamili tunayo na Wabunge kama mtahitaji tutawatolea copy tuwape ili muweze kushirikiana nayo kwa sababu baadhi ya makampuni mengine siyo wakweli katika kufanya kazi, lakini tunayo ambayo tumeainisha yapo makampuni 55 ambayo tumeruhusu yanaweza kufanya kazi na Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa ni ninyi wenyewe Waheshimiwa kuzungumza na yale makampuni na kuweza kukubaliana namna bora ya kuweza kufanya upimaji. Kwa sababu wakati mwingine yale makampuni yanaweza yakapima kwa kutumia rasilimali zao, lakini kuna namna ambavyo Halmashauri inakubaliana nao wawalipe kiasi gani katika kazi wanayofanya au wanaweza wakawasiliana na wananchi moja kwa moja wenye mashamba makubwa, lakini kupitia Halmashauri kujua mpango wenu ukoje katika maeneo yale, wanakubaliana namna ya kulipana katika zoezi hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, milango iko wazi, mashirika na makampuni mbalimbali yapo, yanaweza yakafanya kazi hiyo ni kiasi cha Waheshimiwa kufanya mawasiliano nayo. Orodha ipo kwa yeyote atakayehitaji tutatoa copy ili aweze kujua ni kampuni gani anaweza akafanya nayo kazi. (Makofi)
MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi name niulize swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa tatizo la Mwanza linafanana na tatizo la Tabora Manispaa, Kata ya Malolo na mpaka sasa hawajalipwa fidia ya aina yoyote na wakati huo huo Mheshimiwa Waziri wa Ardhi aliwahi kufika na kutoa agizo. Je, Serikali inasemaje kuhusu kulipa fidia ya hawa wakazi wa Kata ya Malolo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kama nilivyosema katika majibu ya awali ambayo nilikuwa naongezea kwa Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais (TAMISEMI), nimesema Wizara imejipanga katika kupitia; kwa sababu tumekusanya madai haya au migororo na fidia anazozisema mengi yako katika ile orodha tuliyoichukua. Kwa hiyo, tutakachofanya sisi ni kukumbusha taasisi zinazohusika na fidia hiyo ili waweze kulipa, kwa sababu ni nyingi kweli zimekaa muda mrefu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna namna nyingine ya kufanya kwa sababu Serikali haiwezi kulipa fidia ambayo inadaiwa taasisi au maeneo mengine tofauti. Kwa hiyo, tutakachofanya sisi ni kupeleka kumbukumbu za kuwakumbusha wahusika na pale ambapo Serikali inahusika yenyewe basi itajipanga namna ya kuweza kuilipa.
MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya kutia moyo ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Kwa kuwa migogoro ya ardhi katika Halmashauri zetu na hasa Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo imekuwa mingi sana, je, Serikali ina mpango gani wa kuziwezesha ofisi za Kanda ku-speed up utoaji wa hati ili kupunguza migogoro ya ardhi? (Makofi)
Sehemu ya pili, moja kati ya vitu vinavyosababisha migogoro mikubwa sana ya ardhi, hasa mijini ni uwepo wa baadhi ya watumishi wa Idara ya Ardhi wasiokuwa waaminifu katika Halmashauri zetu, watumishi hawa wamekuwa wakikaa muda mrefu sana sehemu moja ya kituo cha kazi. Je, Serikali ina mpango wowote wa kuwabadilisha mara kwa mara ili kujenga mahusiano mazuri kati ya wananchi na watumishi hao wa Idara ya Ardhi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, Wizara imekuwa ikiwezesha Ofisi za Kanda na tuna Kanda nane na zote zinafanya kazi hiyo ya usajili kama alivyosema, pengine labda kama kuna eneo ambalo lina upungufu na kazi hazifanyiki vizuri tungeomba kufahamu, kwa sababu ninavyofahamu mimi Kanda zote nane zinafanya kazi ya usajili na ndiyo maana tumefanya hivyo ili kurahisisha usajili katika maeneo hayo. Kwa hiyo, kama kuna sehemu kuna tatizo basi ni vizuri tukafahamu maaana lengo la Serikali ni kurahisisha na kupunguza ule muda wa kusubiri, kwa sababu sasa hivi ndani ya mwezi mmoja tunasema hati inakuwa imeshasajiliwa. Lakini kama lengo letu halifikiwi maana yake kuna tatizo mahali fulani, sasa nitashukuru sana Mheshimiwa Mbunge kama atatuambia kwamba pengine kanda hiyo ambayo anatoka yeye hakuna ufanisi mzuri katika suala zima la usajili.
Mheshimiwa Spika, swali la pili anasema uwepo wa watumishi wasio waaminifu na wa kukaa kwa muda mrefu.
Mheshimiwa Spika, nadhani ni azma ya Serikali kuona kwamba watumishi wanapokuwa katika maeneo wanafanya kazi zao kwa uadilifu na weledi mkubwa kama ambavyo dhamana hiyo wamepewa. Lakini pale inapotokea pengine mtumishi amekaa eneo moja muda mrefu na amekuwa mzoefu kawa kama ni mwanakijiji katika eneo lile au ni mwanamji wa pale na ameshindwa kufanya kazi aliyoifanya, basi tutawasiliana na Wizara husika ili tuweze kuona nini cha kufanya. Kwa sababu kumhamisha pale kama ameshindwa kufanya kazi na kumpeleka eneo lingine unakuwa hujamsaidia, kama ana tatizo kubwa basi tujue tatizo lake ni nini ili hatua za kinidhamu ziweze kuchukuliwa. Pengine kuwahamisha tu inaweza ikawa siyo solution, lakini kikubwa ni kujua madhaifu yake ni nini ili tuweze kuona hatua za kinidhamu kuweza kumchukulia mtumishi kama huyo.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nakushukuru kwa nafasi, naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri swali moja dogo la nyongeza.
Kwa kuwa utendaji mbovu na kutokuwajibika kwa watendaji wa ardhi waliopo kwenye Halmashauri kunachangiwa pia na muundo mzima kwamba watendaji wale hawapata order wala maelekezo kutoka kwenye Serikali Kuu kwa maana ya kwenye Wizara, na hasa wanapokosea inakuwa ni vigumu kwa Waziri kutoka juu kumchukulia hatua kwa sababu anasikiliza sana kwenye Halmashauri.
Je, Serikali haioni umuhimu sasa, kwa unyeti wa Wizara hii na kuondoa migogoro ndani ya nchi yetu kuhakikisha kwamba watendaji wote wa ardhi wanapokea order kutoka juu na hata wanapokosea waweze kuchukuliwa hatua kutoka juu ili kuondoa migogoro ndani ya nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, utendaji mbovu wa watumishi hasa kwenye sekta ya ardhi nadhani siyo suala tu pia la kujua kwamba anapokea order kutoka mamlaka ipi. Ni kweli katika ule mlolongo uliopo pengine unaweza ukaliona hivyo, lakini nia ya Serikali kugatua madaraka na kusogeza huduma katika Halmashauri zetu ilikuwa ni nia njema na dhamira ya dhati ya kutaka kuona kwamba huduma zile zinafanyika kwa wakati mahali ambapo watu wanahitaji.
Mheshimiwa Spika, lakini hili kama limekuwa ni tatizo, nadhani suala la msingi ni ndani ya Serikali kuweza kuona namna ya kuweza kudhibiti udhaifu huu au utendaji huu mbovu uliopo ili tuweze kujua kwamba hapa kinachotakiwa kufanyika, kama mtumishi ambaye anafanya utendaji wake katika viwango visivyostahili na akitarajia tu kabisa kwamba mamlaka yenye sauti kwake ni mamlaka fulani, hilo halimfanyi yeye asamehewe katika kosa alilolifanya.
Kwa hiyo tunachosema, ugatuaji wa madaraka ilikuwa ni kusogeza huduma, lakini kama suala la kitaaluma au suala la kitendaji linaonekana lina ugumu katika namna ya kudhibiti watendaji hawa, nadhani ni suala la kuongea kati ya Wizara zote mbili husika tukajua ni jinsi gani watu hawa tutaweza kuwasimamia vizuri zaidi ili wafanye kazi zao kwa weledi.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Pamoja na uhaba wa Maafisa wa Ardhi na uhaba wa fedha, lakini zoezi la kupima ardhi nchini limekuwa likisuasua na mahitaji ya wananchi kujenga yamekuwa yakiongezeka, kwa hiyo ukiangalia katika hali ya kawaida wananchi wengi wamekuwa wakijenga katika maeneo ambayo hayajapimwa, sasa nataka kauli ya Serikali, ipi ni kauli ya Serikali juu ya wananchi wote wanaojenga katika maeneo ambayo hayajapimwa na Serikali bado inasuasua kwenye kupima maeneo hayo ya ardhi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kasi ya wananchi kujenga ni kubwa kuliko speed ya Serikali katika kupima maeneo, na ni maeneo mengi ambayo kwa sasa yamekaliwa katika mpangilio usio sahihi na ndiyo maana Wizara imeliona hili na tukaja na programu ile ya miaka mitano ya kuhakikisha kwamba wale ambao wamekuwa na speed kali kuliko Serikali tunajaribu kurasimisha maeneo yao ili wakae katika utaratibu mzuri waweze kutambuliwa na Serikali iweze pia kupata kodi zake kupitia katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, lakini katika kuona hili pia tunalifanyia kazi, Serikali imesajili makampuni, ina makampuni karibu 55 ambayo yanafanya kazi ya upimaji katika maeneo, na upimaji wao wanaofanya wanafanya kulingana na mipango iliyoko katika maeneo hayo kwa maana ya ile mipango miji kwenye yale maeneo, masterplan zao ambazo wameziweka pale.
Kwa hiyo kikubwa tunachosema, kasi ya wananchi ni kubwa, Serikali ina speed ndogo na eneo lililopimwa ni dogo, kwa hiyo tunaomba Halmashauri zilizotayari ziyatumie haya makampuni ambayo tumeyabainisha katika suala zima la upimaji, na nilisema pia wakati najibu swali hili tarehe tisa, nikasema orodha tayari tunayo, Halmashauri yoyote iliyo tayari tuwasiliane ili tuwape ile orodha waweze kufanya mawasiliano.
Mheshimiwa Spika, lengo letu ni kuhakikisha Miji imekaa vizuri na imepangika na tunawaomba wananchi, tunawasihi wasianze kuvamia maeneo ovyo sasa hivi kwa sababu kadri tunavyozidi kuweka mikakati ndivyo jinsi ambavyo wao watakuwa katika hatua nzuri ya kuweza kupangiwa maeneo yao, kwa hiyo wasikimbie sana kwa sababu tayari kama Wizara tunaamua kufanya kazi hii kwa weledi mkubwa.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri sana yenye matumaini kwa wananchi wa Jimbo la Korogwe Vijijini, pia nimpongeze kwa safari alizofanya katika Jimbo langu. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa Naibu Waziri umefika na kuliona shamba hili ambalo limetelekezwa zaidi ya miaka 22, ni kwa nini sasa Serikali isiwakabidhi wananchi wakalitumia kwa shughuli zao mbadala? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa mashamba mengi yamechukuliwa mikopo kwenye mabenki na sasa hivi yametelekezwa, nini kauli ya Serikali kwa yale mashamba ambayo yalichukuliwa mikopo, hayaendelezwi na yametelekezwa mpaka muda huu?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza anataka kufahamu ni lini Serikali itakabidhi sasa wananchi hao mashamba hayo ambayo yametelekezwa muda mrefu ili waweze kuyatumia.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, ni kwamba utaratibu ili uweze kumnyang’anya mtu huyu ni lazima ule utaratibu wa kisheria ufwatwe, na ndiyo maana nimesema katika hatua za awali ambazo Serikali imechukua ni kutoa notice kwa hawa ambao wametelekeza mashamba na siyo huyo mmoja tu, yapo mashamba zaidi ya 22 ambapo baada ya ziara yangu wamepewa notice.
Kwa hiyo, niseme tu kwamba taratibu za Serikali zinaendelea, muda ule ukishakwisha ni jukumu la Halmashauri husika kuweza kupendekeza kwa Mheshimiwa Waziri ili na yeye aweze kumshauri Rais kubatilisha, ni lazima ule mchakato wa kisheria utimizwe. Kwa sababu wenzetu wa Korogwe wameshaanza nina imani litafikia mahali pazuri.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anasema mashamba mengi yamekuwa mapori lakini pia inafahamika kwamba mengine yamechukuliwa mikopo mabenki na nini sasa Serikali inasema nini.
Mheshimiwa Spika, niseme haya yamekuja kuahamika na kuthibitika rasmi baada ya Wizara yangu kuanza kutoa ilani kwa wale ambao wameyatelekeza mashamba yao, lakini kama Serikali tunachofanya sasa ni kuhakikisha tunafanya kazi sambamba na mabenki ili fedha za umma zisipotee, kwa sababu dhamana za hati zile zimewekwa na zimechukuliwa mikopo, lakini pengine mikopo ili haikwenda kunufaisha katika yale maeneo.
Kwa hiyo, jukumu letu sisi tunalofanya, pamoja na ilani zinazotolewa katika mashamba haya, lakini bado kama Serikali tunafanya kazi kwa karibu sana na mabenki ili kuhakikisha kwamba kama zile dhamana walizokuwa wameweka pengine zinakwenda kubatilishwa sasa tujue ni namna gani yale mabenki yataweza kupata pesa zake. Kwa hiyo hili tunalifanya kwa uangalifu ili kuona kwamba pesa za Umma hazipotei lakini pia haki ya wananchi au ya wamiliki wale pia inakwenda sambamba kisheria ili tusijikute kwamba tumekwenda nje ya utaratibu. (Makofi)
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Kwa kuwa suala la mashamba ya mkonge kwa upande wa Korogwe Vijijini inafanana na Korogwe Mjini, na kwa kuwa Korogwe Mjini tayari ilishaingia kwenye mpango kabambe wa masterplan, na kwa kuwa mji huu una mashamba ya mkonge nayo ambayo hayaendelezwi na tayari tulishaleta mapendekezo ya kuomba mashamba hayo yafutwe.
Je, Serikali inatuambiaje na hasa ikizingatia kwamba tupo kwenye ule mpango kabambe wa masterplan kuhakikisha kwamba mashamba hayo yanafutwa ili maeneo hayo yaweze kutumika katika huu mpango kabambe ambao umeandaliwa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba hayo mashamba ambayo tayari wao wameleta mapendekezo kwa Waziri ili na yeye aweze kumshauri Rais ayabatilishe ni yale pia katika mchakato ambayo pengine tunasema kwamba kuna maeneo mengine ambapo wamekopea pesa benki.
Kwa hiyo, mchakato unafanyika ili kuweza kujua, na pale pale tunaangalia ile ilani ambapo kama imekwenda sawasawa kisheria, kwa sababu mashamba ni mengi na yote yanahitaji pia umakini katika kuyabatilisha.
Kwa hiyo, tusingependa kutoa ushauri ambao pengine unaweza ukampotosha Mheshimiwa Rais akaja akalaumiwa, tunataka kujiridhisha na masharti yote yaliyopo pale kama yamezingatiwa lakini pia na kuangalia fedha za Umma zisije zikapotea kwa sababu tu hawa watakuwa wamebatilishiwa umiliki wao.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hilo tunalifanyia kazi na nimwahidi Mheshimiwa Mbunge tutakwenda kuiangalia orodha ya mashamba ambayo anayasema tuweze kuona yamefikia katika utaratibu gani ili hatua nyingine ziweze kuendelea.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niulize swali dogo tu la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, matatizo yaliyopo huko Korogwe yanafanana sana na matatizo yaliyopo katika Jimbo la Itigi; kuna shamba lililokuwa la Shirika la Tanganyika Packers lipo katika eneo la Kitaraka, lilitelekezwa na shirika hili baada ya shirika hili kufilisika mwishoni mwa miaka ya 1980.
Mheshimiwa Spika, wananchi wa maeneo yale katika vijiji vya Kitaraka, Kaskazi Stesheni, Doroto, Majengo, Tambukareli, Kihanju na Sanjaranda wamelitumia shamba lile kulima na linawasaidia sana kupata mahitaji yao ikiwemo mazao ya chakula pamoja na mazao ya biashara, lakini kuna taarifa kwamba Serikali ina mpango wa kulibinafsisha shamba lile kwa wawekezaji.
Je, ni nini kauli ya Serikali kwamba haitaonesha inaleta mgogoro na wananchi ambao shamba lile sasa linawanufaisha wananchi wengi sana wazawa na wananchi wa nchi hii kuliko kuweka mwekezaji, ni nini kauli ya Serikali juu ya suala hilo?
NAIBU WAZIRI ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli anachokizungumza kwamba wananchi wamekuwa wakilitumia lile shamba na ametaja vijiji vinavyohusika. Naomba nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge kwamba nia ya Serikali ni njema na kama kuna hatua ya kuweka mwekezaji vilevile pia itakuwa ni kwa ajili ya manufaa ya wananchi wa Jimbo lake.
Mheshimiwa Spika, tunachotaka afahamu ni kwamba Serikali haiko pale kunyang’anya wananchi ardhi na kuwaacha wakiteseka. Kitakachofanyika ni kwamba watakaokuwa wa kwanza kufikiriwa ni wale wananchi walioko pale na kwa sababu shamba lile lilikuwa linamilikiwa na Serikali tangu awali kwa maana hiyo Serikali kulipangia matumizi mengine ni sahihi. Tutakachofanya kabla halijapewa mwekezaji lazima yale maridhiano ya awali katika kukubaliana namna ya kuweza kufanya ile kazi yaweze kukubalika kwa sababu wao pia wanatambua hawako pale kihalali kulingana na umiliki wa shamba lile.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naitwa Waitara, jina hili inabidi ulifahamu, jina rahisi kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, ameandika mwenyewe hapa kwamba gharama za upimaji ni shilingi 300,000 lakini mimi niliwaita hawa wahusika nikataka wanipimie eneo langu ambalo halifiki ekari mbili, wakafanya tathmini na wakaniambia natakiwa nilipe shilingi milioni tano, kwa hiyo nikapiga mahesabu wananchi wangu ambao wananizunguka pale Kivule na maeneo mengine wanawezaje kumudu hizo gharama kubwa za kupimiwa maeneo yao?
Kwa hiyo naomba kwanza anisaidie, gharama nilizopewa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala ni milioni tano kwa eneo langu chini ya ekari mbili, yeye anasema hekta moja ni shilingi 300,000, na nini kauli yake sasa kwa maana ya maelekezo nchi nzima juu ya hili la upimaji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika maelezo yake Mheshimiwa Naibu Waziri anasema kwamba mimi nimeuliza swali langu ni hatua gani za dharura kwa sasa kwa sababu migogoro mingi ya ardhi iliyopo nchi nzima ni kwa sababu maeneo hayo kwa sehemu kubwa hayajapimwa na ikiwemo Dar es Salaam na watu wanasogeza mawe, kunakuwa na ugomvi mkubwa na kuna kesi nyingi katika mabaraza ya ardhi. Sasa nikataka mkakati wa dharura.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri anasema wana mpango wa kusogeza huduma, sasa naomba anisaidie, huu mpango walionao kuna bajeti yoyote ambayo imetengwa? Kwa sababu wakisema halmashauri inunue vifaa hivi ambavyo yeye mwenyewe amesema ni gharama, kama Waziri anakiri kwamba gharama ya vifaa vya upimaji wa ardhi ni kubwa Halmashauri ambayo haina fedha na imeomba fedha kutoka kwenye Bunge hili na Serikali hawajapeleka mpaka leo, hali ni mbaya, wao Serikali kwa maana ya hii Wizara wanasaidia nini katika mpango wa dharura kwa sasa ili huduma hizi ziweze kupatikana katika maeneo husika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ameuliza maswali mawili, jambo la kwanza amesema, nimetaja kwamba gharama za upimaji ni 300,000 kwa hekta. Naomba niseme hizo ndizo gharama sahihi ambazo tulipitisha hapa kwenye kikao baada ya kupunguzwa ile awali iliyokuwa shilingi 800,000 na Bunge hili lilipitisha baada ya Mheshimiwa Waziri kuleta katika bajeti yake na kuomba ipunguzwe. Sasa kama Manispaa inatozo lingine tofauti na wewe ni mmojawapo katika Manispaa hiyo, ni vizuri pia kujua kwa sababu officially tunachojua na kiko katika maandishi ni shilingi 300,000 lakini kama Halmashauri huwa wana mipango yao kule kutegemeana na Baraza lenyewe la Madiwani wameridhia nini katika lile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwasababu kuna mambo mengine ambayo yanafanyika ndani ya Halmashauri kutegemeana na mamlaka walizonazo, lakini katika rate offial zilizoko ni shilingi 300,000 kwa hekta moja na ni shilingi 300,000 hiyo hiyo kwa kiwanja kimoja. Sasa pengine itabidi tuwasiliane kuweza kujua kwanini wanatoza shilingi milioni tano kwasababu zipi za msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ameongelea habari ya harakati zipi za dharura ambazo tunazifanya ili kupunguza hilo na ni bajeti gani imetengwa. Naomba niseme; bajeti tuliyopitisha hapa Wizara ilileta bajeti ya shilingi bilioni nane kwa ajili ya kununua vifaa hivyo na tayari mchakato wa kununua umeshaanza na kwa sababu uko chini ya Benki ya Dunia ambao ndio wafadhili, mchakato ndani ya Wizara tumeshamaliza, tunachosubiri tu ni ile no objection kutoka Benki ya Dunia, wakishapitisha sisi hatuna tatizo kwasababu tayari ipo na tulisema itakwenda katika kanda zote nane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, harakati za dharura ambazo tunafanya sisi ndiyo katika hizo lakini bado tulishasema kuna makampuni zaidi ya 58 ambayo yapo na Halmashauri inaweza kuyatumia, Wizara imesharidhia yafanye kazi hiyo ili kuondokana na tatizo hili. Kama Wizara tunafanya kazi ya urasimishaji katika maeneo ambayo hayako vizuri, kwahiyo hilo naweza kujibu kuwa ndizo hasa harakati zetu tunazofanya kuhakikisha tatizo hilo linaondoka.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kama kuna maamuzi mabaya yalishawahi kufanyika ni maamuzi tuliyoyafanya katika Bunge la bajeti hii iliyopita ya 2016/2017 kwa kuondoa au kufuta vyanzo vikubwa ambavyo vinazipatia Halmashauri mapato na kuvipeleka Serikali Kuu.
Mfano kodi ya majengo ambayo mpaka sasa TRA wameshindwa kukusanya, kodi ya ardhi inapelekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina lakini mpaka sasa hazijarudishwa, Halmashauri hazina fedha. Swali, Mheshimiwa Waziri ni kwa nini msifikirie upya uamuzi huu na kurudisha vyanzo hivi kwenye Halmashauri zetu kwa sababu hata Serikali Kuu mkikusanya hamzirudishi kwa wakati? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri juzi hapa kwenye Bunge hili kwamba Halmashauri zetu nyingi hazina set za upimaji viwanja, hakuna vile vifaa na katika majibu yake amesema kwamba ataangalia utaratibu wa kurudisha fedha hizi. Ni kwa nini sasa hizi pesa zisitumike kununua vifaa vya upimaji katika Halmashauri zetu ilhali amekiri mwenyewe kwamba hakuna vifaa hivyo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ambalo ameanza na maelezo anasema kwamba kama kuna maamuzi mabaya yamefanyika ni Bunge la bajeti lililopita. Mimi niseme tu maamuzi ya Bunge yaliyopitishwa na yeye ni mhusika kwa sababu ni mmoja wa Wabunge waliopitisha.
Maana yake ni kwamba Bunge linapoamua Wizara inatekeleza yale ambayo yanakuwa yameamuliwa kwa sababu yanakuwa na manufaa kwa Taifa. Kwa hiyo, sisi tunatekeleza kile ambacho Bunge hili liliona kinafaa kuzingatiwa kwa ajili ya mustakabali wa maendeleo ya Taifa hili kwa ujumla wake. Kwa hiyo, hayo ni maamuzi ya Bunge na tunayafanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili amezungumzia suala la gharama za vifaa na nilisema hapa wazi ni kweli na tulitaja mpaka na gharama zake kwamba ni kubwa. Katika utaratibu mzima wa kuziwezesha Halmashauri zetu, Wizara kama Wizara kwa sasa na juzi nilisema hapa kwamba tayari tumeshatangaza zabuni ya kununua vifaa vitakavyokwenda katika ofisi zetu za kanda na zitafanya kazi katika Halmashauri zile. Wizara kuwa na vifaa katika kanda haizuii Halmashauri zenyewe kuweka mpango wake wa kununua vifaa kwa ajili ya kufanya kazi. Wizara inasaidia kuhakikisha kwamba kazi zile zinafanyika katika maeneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa sababu suala hili linaonekana ni tatizo na ni changamoto kubwa, ndiyo maana nimesema kwa utaratibu wa sasa Wizara yangu pamoja na Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunaangalia namna bora ya kuhakikisha kwamba idara hii haishindwi kufanya kazi zake katika Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wakati Wizara inaangalia namna bora ya kufanya, basi pia ni jukumu la Halmashauri zetu kuona ni namna gani tutaliwezesha zoezi hilo ili tuweze kufanya kazi za upimaji na kazi za ardhi kwa ujumla ziweze kufanyika vizuri.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo bado hayajaridhisha sana kwa sababu maeneo mengi wananchi bado wanajenga kiholela. Wakishajenga kiholela baadaye ndiyo Serikali inajua kuwa hawa wamejenga kiholela wanaanza kuja kuwasumbua, kunakuwa hakuna barabara hata watu wakiugua kwa mfano akinamama wajawazito jinsi ya kutoka maeneo yale kwenda hospitalini inakuwa shida kwa vile usafiri hauingii katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali inaona jambo hili kuwa wananchi wanajenga kiholela na baadaye inakuwa shida na tabu, lini sasa itaweka mipango mikakati ya kuhakikisha inapima kwanza halafu inawagawia wananchi viwanja ili waweze kupata maeneo mazuri na yenye kupitika? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwa kuwa Manispaa ya Mpanda kuna migogoro mingi sana ya ardhi na nilishamwambia Waziri aje Mpanda kuona jinsi wananchi wanavyopata tabu. Je, ni lini sasa mimi na yeye tutaongozana kwenda Mpanda ili aende akatatue matatizo ya wananchi wa Mpanda?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ameanza kwa maelezo na kusema kwamba Serikali inaacha watu wanajenga holela na baadaye inakuja kuwabomolea, lini itaweka mpango mkakati wa kupima ardhi yote? Kama Wizara tayari tumekwishaanza zoezi hili na tulilitambulisha pia wakati wa bajeti na tumeanza na Mkoa wa Morogoro katika zile Wilaya tatu za Ulanga, Kilombero na Malinyi. Huko ndipo tulipoanzia na uzoefu mzuri utaonekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hii haizuii Halmashauri kufanya mipango yake ya upimaji wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo yao. Kwa sababu kama itaachiwa Wizara peke yake haiwezi kupima kwa wakati na ikamaliza kwa nchi nzima hii. Ndiyo maana kama Halmashauri tunacho kitengo/idara yetu, mipango miji wako pale ambapo wanatakiwa pia kuangalia namna ya upangaji miji. Ndiyo maana sasa hivi tuna miji zaidi ya 33 ambayo wameandaa mipango yao kabambe ili kuweka miji salama. Vilevile ujenzi unafanyika kule kwenye Halmashauri zetu, kwa hiyo kama Halmashauri tunapaswa pia kulisimamia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai tu kwamba zoezi hili tunapaswa wote kushirikiana kuweza kuangalia watu wanawezaje kuendeleza makazi yao vizuri na kwa kuzingatia sheria kwa sababu tuko nao karibu zaidi katika Halmashauri zetu. Kwa hiyo, tunalichukua kama changamoto, lakini bado tunalirejesha kama changamoto pia kwenye Halmashauri zetu kuweza kusimamia matumizi bora ya ardhi katika maeneo yao na kama mipango haijapangwa basi iweze kupangwa. Wataalam wa Wizara yangu wapo wanaweza wakasaidia kikanda kupanga matumizi bora ya ardhi ili kuwaondolea wananchi hawa kero ambayo wanaipata pale ambapo wanabomolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ameongelea migogoro ya Mpanda na alitutaka twende. Nadhani tulizungumza kwamba migogoro iliyopo ni mingi na kama Wizara tumeipokea. Juzi wakati tunajibu swali hapa tumesema tunayo timu maalum inayoandaa tathmini ya ile migogoro. Kwa sababu unapofunga safari huwezi kwenda kufanya kazi ya mgogoro mmoja halafu ukarudi. Tunataka unapokwenda mahali uende ukaipitia migogoro yote iliyopo lakini pia uwe umeshapata ABCs za ile migogoro na chanzo chake, ukifika kule unatoa ufumbuzi wa kudumu na siyo kwenda tena halafu kurudi mara nyingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, zoezi hili la kwenda kwenye maeneo baada ya muda si mrefu tutawatembelea na tutafika kwa sababu timu inayoandaa tathmini ya ile migogoro na kuweka mapendekezo na kupitia zile taarifa za zamani za tume mbalimbali ili tuweze kuzifanyia kazi, karibu inakamilisha kazi yake na ikikamilika utaona tutafika na niko tayari kufika kwenye eneo lake.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nimesikiliza majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ambapo amesema hivi sasa Serikali ime-stick kupima kwenye Sh. 300,000/= kwa hekta moja lakini pia amesema Serikali inashirikiana na wapima binafsi. Je, Serikali imeweka mikakati gani ya kuzuia hao wapima binafsi wasiendelee kuongeza bei kwa maana ya kuwaumiza wananchi ambao wanahitaji huduma hii ya kupimiwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Serikali inasema nini juu ya wananchi wa Mtaa wa CCT Mkundi katika Manispaa ya Morogoro ambao walifuata taratibu zote za kupata hati, lakini hivi sasa wamevunjiwa nyumba zao na wengine wanalala nje huku wakiwa na hati zao mikononi. Je, Serikali ina mpango wowote wa kulipa fidia kwa wananchi hao ambao wana hati?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ameuliza habari ya Serikali imeweka mikakati gani kuweza kudhibiti hawa wapima binafsi ili wasiwe na bei ambazo zinaumiza wananchi. Serikali inaweka viwango kutegemeana na hali halisi ya bei inayotakiwa kutozwa mwananchi wakati wa upimaji. Sekta binafsi nayo ipo na inafanya kazi hiyo kwa kushirikiana na Serikali na ndiyo maana juzi tu walikuwa na mkutano wao ambao uliwakutanisha wapima wote ambapo hili pia lilijitokeza kama kero kwa wananchi wengi ambao wanalalamika kwamba gharama zao ziko juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kinachofanyika ndani ya Serikali, kwanza ni kuzungumza nao na pengine kuweza kuelekeza bei ambazo zitaweza kutumika ili kutompunja au kumuumiza zaidi mwananchi. Kwa sababu ukishaachia soko huria wale wanakwambia wana gharama nyingi na kubwa kama ambavyo tumesema vifaa vyao jinsi vilivyo, lakini kama Serikali hatuwezi kuwaachia waendelee kulitawala soko na wakati huohuo tunahitaji ardhi iwe imepimwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Wizara tunajadiliana nao na nadhani Waziri aliongea nao na akaelekeza vizuri nini cha kufanya ili waweze kuja na taratibu ambazo hazitamuumiza mwananchi wa kawaida. Kwa sababu gharama za upimaji zinafahamika na wao wasiwe na visingizio vya kutaka kutoza fedha nyingi bila sababu ya msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama tulivyokuja kwenye bei ya viwanja, vivyohivyo na gharama za upimaji lazima nazo zitakuwa na bei elekezi pamoja na kwamba ni soko huria, lakini ni bei ambazo zinalinda mlaji ili kuondokana na tatizo hili. Lengo letu ni kuhakikisha ardhi yote imepimwa. Gharama ni kubwa lakini na Wizara haiwezi kupima ardhi yote peke yake bila kushirikiana na taasisi binafsi, inaweza ikawa ngumu zaidi. Kwa hiyo, naomba mtupe muda, tunazungumza nao tuweze kufikia muafaka namna gani ya kuweza kutoza gharama za upimaji kwa maeneo yote hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ameongelea habari ya wale ambao wamevunjiwa na walifuata taratibu. Serikali ilishaelekeza, kama kuna watu walikuwa na hati na walizipata kihalali, watu wale walitakiwa kutambuliwa. Kwa sababu zoezi hili ni kama lile lililofanyika Dar es Salaam ambapo Wizara ilielekeza wale waliokuwa na hati za halali za umiliki walitakiwa kuleta hati zao Wizarani wakatambuliwa. Kwa hiyo, hili linaweza likafanyika hivyohivyo na Morogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Morogoro tuna ofisi yetu, wapeleke hati zao tuweze kuzipitia, kama zilikuwa ni halali basi tutaona nini cha kufanya, kama ni viwanja vingine au kufuata utaratibu mwingine. Kwa sababu wakati mwingine kuna watumishi ambao hawakuwa waaminifu, anaweza akawa anasema ana hati kumbe hati yenyewe siyo halali. Kwa hiyo, tutazipitia zile hati zote, aliyekuwa na hati halali amevunjiwa kimakosa, basi taratibu za kisheria zitazingatiwa na atapata haki yake.
MHE. SALMA M. MWASSA: Mheshimiwa Spika ahsante. Pamoja na majibu ya kuleta matumaini ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika Sheria hii ya Mabaraza ya Ardhi inasema kwamba; Baraza la Ardhi la Wilaya lisiongelee kesi inayozidi au kiwanja kinachozidi thamani ya shilingi milioni 50, na Baraza la Nyumba la Kata lisiongelee kiwanja au nyumba inayozidi shilingi milioni tatu.
Meshimiwa Spika, kwa mikoa kama Dar es Salaam, Mwanza, maeneo yoye ya mijini Nyumba nyingi zimezidi thamani ya shilingi milioni 50. Sasa kutokana na sheria hii kutokukidhi matakwa halisi ya mwenendo wa thamani ya ardhi iliyopo mijini kwa sasa, ni lini sheria hii itarekebishwa au iletwe hapa Bungeni irekebishwe au ifanyiwe amendment ili iendane na hali halisi ya sasa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, migogoro mingi ya ardhi ya ardhi nchini inasababishwa na ardhi kutopimwa na kumilikishwa kwa ufasaha, na hii inasababishwa na gharama kubwa na mlundikano wa kodi ya umilikaji wa ardhi kwa wananchi.
Mheshimiwa Spika, kwa mfano kodi ya premium katika umilikaji wa ardhi ambayo ni asilimia 7.5 ni kubwa mno kwa sasa, ni lini kodi hii itashushwa au itafutwa ili kuwaletea tija wananchi au kuwapunguzia mzigo wananchi katika kupata haki yao hii ya kumiliki ardhi kwa sasa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza anazungumzia sheria kutokidhi kwa mana ya kwamba viwango vilivyopo kwa sasa na hasa mijini ukiangalia kwa Mabaraza ya ardhi kiwango chake ni shilingi milioni 50 lakini nyumba nyingi zimezidi.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu haya masuala yanakwenda kisheria, na kama hitaji linaonekana kwamba sheria imepitwa na wakati nadhani ni wakati muafaka pengine wa kuweza kupitia upya na kuweza kuangalia kwasababu kadri siku zinavyokwenda ndivyo jinsi na majengo yana-appreciate value zake.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili ni wazi kweli anavyolisema limepitwa na wakati, lakini bado pale inapoonekana kwamba viwango, au kiwango cha kesi husika kinazidi Mamlaka ya Baraza husika kesi hiyo huwa inapelekwa kwenye mahakama ya juu. Kwa hiyo bado linaweza kufanyika wakati bado tunasubiri kubadilisha sheria hii.
Mheshimiwa Spika, suala la pili ni suala la viwango. Tukumbuke katika bajeti nadhani ya mwaka 2015/2016 kiwango cha premium kilishuka kutoka asilimia 15 kwenda kwenye asilimia 7.5. Sasa tuna miaka kama miwili tu toka hii imeanza kutumika na bado inaonekana ni kubwa. Lakini tukumbuke pia kwamba viwango vingi vya ardhi ambavyo vilikuwepo vilishushwa ikiwepo hata ile ya upimaji wa ardhi kwa kiwanja kutoka shilingi 800,000 kwenda shilingi 300,000. Kwa hiyo, haya yote ni mapitio yanayofanyika kulingana na muda jinsi ulivyo.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu hili nalo bado linaonekana ni tatizo siwezi kuahidi hapa ni lini tutaleta sheria hiyo kwa sababu ndiyo kwanza imeanza. Lakini tutazidi kufanya utafiti wa kina na kuweza kujua kama kweli ni kikwazo kikubwa tuweze kuona namna gani tutapitia tena viwango vyetu ili wananchi ambao tunategemea wanufaika wa ardhi hii ambayo sehemu kubwa haijapimwa waweze kunufaika na kupata ardhi zao na kuweza kupata hati ili waweze kufanya shughuli zingine za maendeleo.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na juhudi za Serikali ambazo nazipongeza sana lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa Serikali ina mfuko ambao unawapa watumishi wa Serikali mikopo ya muda mrefu ya nyumba, watumishi hao ni pamoja na walimu. Lakini naweza kusema kwamba mfuko huo haupo wazi kwa walimu wote Tanzania na wala kwa watumishi wengine. Je, Serikali imejipanga vipi sasa katika kutoa elimu juu ya mfuko huu ambao unatolewa mikopo yaani mikopo inayotolewa kwa Serikali imejipanga vipi kutoa elimu kwa walimu na watumishi wengine wa Serikali ili waweze kufaidika na mkopo huo wa nyumba wenye gharama nafuu? (Makofi)
Swali la pili; Kwa kuwa Serikali imeonyesha wazi dhamira ya kutaka kuwasaidia walimu na watumishi wengine kupitia Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii lakini mifuko hii inajenga nyumba zenye gharama kubwa sana kuanzia milioni 50 kwenda juu mpaka milioni 75 gharama ambazo mwalimu wa kawaida hawezi kuzimudu.
Je, kwa nini Serikali sasa isiwashawishi Mifuko hiyo ya Jamii ikatoa mikopo ya fedha taslimu kwa walimu waweze kujijengea nyumba zao wenyewe kwa gharama nafuu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza alitaka tu tutoe elimu kwa ajili ya walimu kufahamu kwamba kuna mfuko ambao unawawezesha wao kuweza kupata mkopo kwa ajili ya nyumba.
Naomba niseme kwamba mfuko huu tulionao Serikalini siyo kwa ajili ya walimu tu, ni mfuko kwa ajili ya watumishi ambao wanaweza kukopeshwa kupitia mfuko wa Serikali.
Kwa hiyo, elimu ambayo tunaweza kuitoa ni pamoja na sisi wenyewe Wabunge kuweza kutoa elimu hii katika Halmashauri zetu kupitia vikao vyetu vya Mabaraza ya Madiwani ili waweze kuwafahamisha pia walimu huko waliko pamoja na watumishi wengine wa kawaida kwamba wanaweza wakapata fursa hiyo kupitia Serikalini. Kwa hiyo, hili ni la kwetu tumelichukua pamoja lakini tushirikiane wote ili kuweza kufikisha ujumbe huu.
La pili, dhamira ya hizi Hifadhi za Jamii katika ujenzi wa nyumba anasema zina gharama kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba nimezungumzia suala la Watumishi Housing ambalo ni Shirika ambalo limeanzishwa na Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii na Shirika hili linatoa nyumba zake kwa gharama nafuu wala hazina gharama kubwa sana isipokuwa masharti yake yalipo ni lazima kwanza uwe na dhamana ambayo inaweza ikakusaidia katika kuweza kurudisha mkopo ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mabenki yale ambayo yanatoa mkopo huu once ukishakubaliana na benki kwamba sasa unataka kuchukua mkopo, Shirika ndiyo linawasiliana na wewe katika hali halisi ya kutaka kujenga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninachotaka kusema ni kwamba nyumba zinazojengwa ziko katika size mbalimbali, kwa hiyo bei ya nyumba na gharama yake itategemea pia na ukubwa wa nyumba. Kwa hiyo, tunapokuwa na mashirika mengi yanayofanya shughuli za ujenzi, ushindani utakuwepo lakini na ubora wa nyumba utakuwepo. Kwa hiyo, itakuwa ni juhudi ya mtu mwenyewe na kuweza kuchagua ni shirika lipi unataka wewe likujengee nyumba katika gharama ile ambayo unaweza, lakini nyumba ziko za gharama nafuu kulingana na vipato vya wananchi wetu.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ningependa tu kufahamu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri kwamba pamoja na mikakati hii mizuri ambayo Serikali inayo katika kuwasaidia watumishi wakiwemo Walimu kupata mikopo ya muda mrefu, sasa ni lini Serikali itazishauri au itazielekeza hizi Halmashauri zetu zote nchini kuhakikisha kwamba kila zinapofanya zoezi la upimaji wa ardhi Walimu wanapewa kipaumbele katika kupata maeneo ambayo pamoja na mkopo watakaopata basi ardhi isiwe kikwazo kwao na waweze kumudu ujenzi huu wa sasa? Nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake anataka kujua ni lini Walimu watapewa kipaumbele kuweza kupewa viwanja pale ambapo Halmashauri zinapima. Ninachoweza kusema tu ni kwamba mipango ya upimaji katika Halmashauri zetu tunaiandaa wenyewe katika vikao vyetu. Kwa hiyo, katika kutoa vipaumbele kwenye kupima, nadhani kwa sababu tumeona kwamba Walimu wana tatizo kubwa ni jukumu letu pia kuhakikisha kwamba tunapopima maeneo basi tunatenga kwa ajili ya watumishi na si Walimu tu kama ambavyo tunavyofanya katika Wizara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo pale ambapo panakuwa pana hitaji kubwa, ni jukumu letu sisi wenyewe kuweza kusema sasa tunapima viwanja sehemu fulani tunawapa watumishi. Kwa upande wa Mwanza, tayari kuna viwanja zaidi ya 500 ambavyo vilipimwa kwa ajili ya watumishi wote kwa ujumla na sio Walimu tu. Kwa hiyo hii inawezekana inaweza kufanyika, ni mipango ya Halmashauri husika.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza Mheshimiwa Naibu Waziri katika sehemu (a) ya swali hajajibu swali. Niliuliza ni lini hii fidia ya hisani italipwa lakini hajajibu ni lini na Mheshimiwa Lukuvi, Waziri wa Ardhi anafahamu kwamba jambo hili ni la muda mrefu. Mwaka 2009 aliyekuwa Waziri wa Ardhi wakati huo Chiligati aliahidi wangelipwa milioni tisa, hawakulipwa mpaka mwaka 2015 wananchi wakaandamana kwenda Wizarani, Serikali ikaahidi kulipa milioni mbili badala ya ile milioni tisa. Sasa sehemu (a) ni vyema Waziri akajibu ni lini hasa Serikali italipa hii fidia. Au inataka sasa kwa kuwa wakati ule tuliandamana kwenda Wizara ya Ardhi sasa tuandamane kwenda kwa Mheshimiwa Magufuli ajibu ni lini hasa hii fidia italipwa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sehemu (b) ya swali. Serikali imesema kwamba haidaiwi mapunjo ya fidia ya maendelezo. Hili jibu la Serikali ni jibu la uongo. Mwezi Aprili mwaka 2014 tulikuwa pamoja na Rais Dkt. Jakaya Kikwete pale Mloganzila, jambo hili likajitokeza na Rais akataka vielelezo tukamkabidhi na sio Rais tu, Wizarani kuna nakala za fomu za watu ambao kimsingi walipunjwa fidia za maendelezo kinyume kabisa na thamani halisi ya mali zilizokuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu Serikali imejibu uongo hapa Bungeni; je, Serikali iko tayari kurudi kwenda kuchunguza malalamiko ambayo yako tayari Wizarani? Vielelezo vyote viko Wizarani na ikalipa fidia ya maendelezo pamoja na kujibu maswali kwa ukweli?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nilijibu swali lake (a) analosema kwamba sikulijibu. Nadhani katika majibu ya awali nilipojibu sehemu (a) na (b) nimesema kwamba watalipwa baada ya kupatikana fedha na hii haijalipwa kutokana na ufinyu wa pesa sasa siwezi kuweka commitment ya Serikali hapa wakati natambua wazi kwamba haya mambo yanakwenda kwa bajeti kama halipo katika bajeti siwezi kukwambia ni kesho tutalipa au kesho kutwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo nilitaka kutoa ufafanuzi huo. Kwa sababu ukisema unaweka commitment leo na pesa haijapatikana, atakuja kusema baadaye kwamba tumedanganya Bunge na sisi hatutaki kulidanganya Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yangu pia hakuna mahali ambapo tumedanganya Bunge. Kwanza kwa sababu hata hao unaowasema wamekuwa wakija sana ofisini wakidai madai yao na tunawaambia nini kilikwisha fanyika na mpaka sasa kitu gani ambacho wanadai. Lakini ukiangalia pale hakuna mapunjo ambayo wanatakiwa walipwe isipokuwa ile iliyosemwa ya hisani ambayo tunasema watakuja kulipwa baada ya kupatikana ndiyo hiyo ambayo Serikali inaifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hatuwezi kusema kwamba kuna watu walipunjwa na ukizingatia kwamba eneo lile ambalo watu wanalipigia kelele bado ilikuwa ni sehemu ya Serikali. Ilikuwa ni viwanja vya Serikali isipokuwa kulikuwa na vijiji vilivyokuwa vinatambulika mle na ndiyo maana Serikali ikawa tayari kulipa fidia ya maendelezo katika yale maeneo waliyokuwa nayo.
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na pongezi zangu kwa niaba ya Wanauyui na Tabora wa ujumla kupeleka Msajili wa Hati, nina maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, kwa vile kuna upungufu mkubwa sana wa idara mbalimbali za ardhi pale ikiwemo ya upimaji na mipango: Je, Serikali iko tayari kupeleka tena wataalam hao ili wafanye kazi na Msajili huyu wa Hati?
Swali la pili; kwa vile kabla ya kupelekwa Msajili huyu wiki moja iliyopita, kwa miaka mingi iliyopita Hati za Tabora zimekuwa zinasajiliwa katika Ofisi nyingine za Kanda, Dodoma na Mwanza: Je, Serikali sasa iko tayari kurudisha kumbukumbu ya Hati zetu zote pale Tabora? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameuliza kuhusu upungufu wa wataalam wa idara nyingine, ametaja mipango miji, kama tuko tayari kupeleka.
Mheshimiwa Spika, naomba nilihakikishie Bunge lako kwamba kwa sasa katika kipindi hiki ambacho pia tunatakiwa kama Wizara zote au Serikali kuhamia Dodoma, baadhi ya Wataalam ambao wako Makao Makuu tutawasambaza katika kanda ambazo zina upungufu, kwa sababu, maeneo mengi ni karibu yanao wataalam wa kutosha, lakini ni machache likiwepo la Tabora ambao hawana wataalam hao. Kwa hiyo, tutawapeleka katika Kanda ili kuendelea kuziimarisha kama tulivyoahidi.
Mheshimiwa Spika, jambo la pili, amesema Hati zilizoko Mwanza na maeneo mengine ambazo ni za Tabora; naomba nimhakikishie tutafanya utaratibu wa kuhakikisha hati hizo zinarudi katika ofisi husika kwa sababu tayari Msajili ameshapatikana, basi anao wajibu pia wa kuhakikisha anatunza Hati za Maeneo ambayo anayasimamia na yeye wa Kanda ya Tabora ana Mikoa zaidi ya minne.
MHE. SAVELINA S. MWIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa nyumba nyingi zimefanyiwa ukarabati kama alivyosema Naibu Waziri, Bukoba Mjini kuna majumba ya NHC yaliyochakaa yanaonesha Mji kuchafuka kwa ajili ya nyumba hizo za NHC.
Je, ni lini Serikali itafanyia ukarabati au kujenga
majengo mapya ya NHC?
Swali la pili, kuna majengo ambayo yamechakaa yako kwenye mtaa wa Miembeni watu wameishi muda mrefu hayana miundombinu hayana sehemu za kuingilia watu wenyewe waliopanga mle ndio wanajiwekea miundombinu na Serikali inakusanya ushuru na inakusanya kodi za majengo.
Je, ni lini Serikali itajenga nyumba mpya au
kuwaruhusu wale waliomo ndani kuzinunua?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwijage amezungumzia suala la ukarabati wa nyumba za Bukoba zilizo chakavu. Kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi nimesema suala la ukarabati ni suala endelevu na pale ambapo nyumba zinaonekana zimechakaa haziwezi tena kufanyiwa ukarabati, shirika linabomoa nyumba zile na kujenga majengo mengine mapya.
Kwa hiyo, niseme kwamba kama nyumba za Bukoba anavyosema kwamba zimechakaa, zinahitaji ukarabati nadhani bado tutaangalia kwa sababu Meneja yupo pale anaziona na anajua na ndiyo maana nimesema ukarabati huu unaendelea nchi nzima, kwa hiyo na Bukoba pia ni moja ya eneo ambalo litaangaliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili eneo la Miembeni nyumba zilizoko ni chakavu na hazina miundombinu. Kama nilivyosema jibu la msingi kama ni chakavu na haziwezi kufanyiwa ukarabati nadhani jukumu lililopo ni kubomoa na kujenga nyumba nyingine mpya na watu wakakaa katika mazingira yaliyo mazuri. Hatakubali kuendelea kuwa na nyumba ambazo ni chakavu na hazina
uwezekano wa kufanyiwa repear. Kwa hiyo, ni jukumu la Shirika la Nyumba tutawatuma waende waangalie hizo ambazo hazina miundombinu na haziwezi kukarabatika tena tuone utaratibu wa kuweza kuzijenga upya katika hali hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, umilikishaji kwa wananchi ni kwamba sasa hivi kuna ule utaratibu wa mpangaji mnunuzi, kwa hiyo, kuna maeneo ambayo kuna hizo nyumba ambazo zinajengwa bado mpangaji anaweza kuwa mnunuzi kwa hiyo mtu atamilikishwa nyumba pale atakapokuwa amelipia nyumba yake na amefikia mwisho wa gharama ya nyumba husika.
MHE. ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona na mimi niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa lengo la kuboresha nyumba hizi za National Housing ni kuwaondolea bugudha wapangaji wanaoishi katika nyumba hizo; sasa pale kwenye nyumba zilizoko Keko Juu, Kata ya Keko njia panda ya kwenda Uwanja wa Taifa wapangaji katika nyumba nne kati ya nyumba Nane zilizokuwa pale waliwahi kupewa notice ya kutaka kuhama bila sababu za msingi na wapangaji wakaamua kwenda mahakamani. Mpaka tunapozungumza sasa kesi hiyo ipo mahakamani. Mahakama imesema kwamba wakati kesi bado inaendelea pande zile mbili kati ya National Housing na wapangaji sizibughudhiane, lakini mara kwa mara...
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja kwenye swali. Kinachoendela sasa kila baada ya muda mfupi National Housing wanawatuma madalali kupeleka notice kwa wapangaji wale. Kwa kuwa, kesi ipo Mahakamani na kuwapelekea notice ni kuwabughudhi wapangaji wale na kuingilia Mahakama, Mheshimiwa Waziri anaweza kutoa kauli hapa leo ya kuwaambia National Housing waache kuwabughudhi wapangaji wale mpaka kesi itakapoisha?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba Wizara kama Wizara haiwezi kutoa kauli hapa kwa maamuzi ambayo yako nje ya muhimili wa Bunge. Maamuzi ya Mahakama yatabaki kama yalivyo na kwa maana hiyo yale yaliyoagizwa na Mahakama ndiyo yatakayoendelea kuheshimiwa mpaka hapo uamuzi sahihi utakapokuwa umetoka.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa imeshatenga eneo ambalo Shirika la Nyumba la Taifa wanatakiwa kujenga nyumba, sasa ni miaka miwili.
Je, Shirika la Nyumba bado lina mpango wa kujenga nyumba kwenye Mji wa Maswa au mpango huu umesitishwa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, National Housing bado inayo dhamira ya dhati ya kujenga nyumba katika maeneo yetu kwa nchi mzima na hasa pale Halmashauri zenyewe zinapokuwa ziko tayari zimetenga maeneo kwa ajili ya kazi hiyo. Kwa eneo na Maswa bahati nzuri nilifika na nafahamu eneo lilipo bado dhamira ya Shirika iko pale pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo kubwa ambalo
linatakiwa kufanyika kwa sababu mara nyingi pia tumekuwa tukilalamika kuwa bei ya nyumba kuwa kubwa, sasa Halmashauri ambazo zina maeneo kama Maswa wanatakiwa kuwa wamefanya maandalizi ya miundombinu katika maeneo yao, ikiwepo suala la barabara, suala la maji na suala la umeme ili watakapo kuja kujenga zile nyumba basi ziwe na gharama nafuu kama ambavyo inatarajiwa kuwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo napenda
kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba dhamira ya shirika bado ipo pale pale kujenga nyumba kwa kihakikisha Watanzania wanakuwa na makazi bora.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri na nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa tatizo hili la migogoro baina ya wakulima na wafugaji siyo la Mkoa wa Morogoro peke yake, tumelishuhudia katika Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Lindi, sasa kwa nini Wilaya zote tatu za majaribio zimekuwa katika mkoa mmoja? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pili, je, Mkoa wa Pwani na Lindi
zoezi hilo litafanyika lini ili kuondoa changamoto ya wakulima na wafugaji hasa katika Wilaya za Rufiji, Kilwa na yale maeneo ambayo wafugaji wapo kwa wingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwanza napokea pongezi zake ambazo ametoa na mimi nashukuru, ni kutokana na ushirikiano wetu sote. Katika maswali yake mawili aliyozungumza; la kwanza, amesema tatizo la migogoro lipo katika mikoa mingi nchini na kwa nini tumeamua kuanzia Mkoa wa Morogoro peke yake na Wilaya zote tatu za mfano zipo Mkoa wa Morogoro?
Mheshimiwa Spika, napenda nilithibitishie Bunge lako hili, nadhani wote ni mashahidi kwamba katika ile migogoro ya wakulima na wafugaji kwa Mkoa wa Morogoro ilikuwa ni kama imekithiri.
Mheshimiwa Spika, mauaji mengi yalikuwa yanatokea kule na kila leo kulikuwa na changamoto za hapa na pale na ndiyo maana tukasema sasa kwa sababu maeneo hayo yamekuwa na mgogoro mkubwa tuanzie pale ili tuweze kupata uzoefu pia wa kuweza kutatua migogoro ya aina hiyo katika maeneo mengine.
Kwa hiyo, kuanzia Morogoro lengo lake kubwa ilikuwa tu ni katika kuhimili ile migogoro iliyokuwepo na kuona namna gani tutaweza kuisitisha ili tuweze kufanya kazi hii vizuri zaidi katika maeneo mengine.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anasema, ni lini tutakwenda katika Mkoa wa Pwani na Lindi na hususan Rufiji na Kilwa, kama alivyotolea mfano.
Mheshimiwa Spika, naomba niseme tu, kwa sababu utatuzi wa migogoro hii na upangaji na upimaji utafanyika kwa awamu mbili na tumekwishaanza, mimi niseme pale ambapo tutakuwa tumepanga ratiba inayofuatia, basi tutaweka na mikoa ambayo ina migogoro ukiwemo na Mkoa wa Pwani ambao nao pia unaonekana una migogoro mikubwa.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutafanya hivyo kutegemeana na uzoefu tulionao katika migogoro iliyopo lakini pia katika kuhakikisha migogoro mingine haiibuki.
MHE. UPENDO F. PENEZA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Wizara inatambua kwamba makazi duni huchangia katika kuleta afya mbovu kwa wananchi. Ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi yake ya kupunguza kodi kwenye vifaa vya ujenzi ili sasa wananchi waweze kujenga nyumba bora na kuepukana na nyumba za tembe na nyasi?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, Sheria ya Madini
ya Mwaka 2010 inaongelea suala la resettlement; kwa wananchi wanaotokana na maeneo ambayo yana shughuli nyingi za wawekezaji, wakilipwa fidia hulipwa pesa na kuondoka, Sheria ya Madini ya mwaka 2010 inazungumzia kwamba ahamishwe na ahakikishe kama alikuwa na mwembe, basi ataachana naye pale ambapo mwembe utakuwa umeota na kuanza kuzaa. Ni lini sasa Serikali italeta ndani ya Bunge hili mabadiliko ili Bunge liweze kufanya mabadiliko katika Sheria ya Ardhi ili sasa hilo suala la resettlement liweze pia kuzungumziwa katika Sheria ya Ardhi ili wananchi wapate fidia ambayo ni sahihi na waweze kunufaika na uwekezaji huu ndani ya nchi yetu? Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza amezungumzia hali duni ya makazi ya watu na kufanya pengine wasiwe na makazi bora, pengine yanachangiwa labda na vifaa kuwa na bei ya juu.
Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala la kupunguza kodi katika vifaa vya ujenzi ni suala ambalo linahitaji kupitiwa kwa upya katika utaratibu wake kwa sababu mwanzo Waheshimiwa Wabunge walileta suala la kutaka kupunga VAT katika vifaa vya ujenzi, lakini lilikuwa limelenga eneo moja. Katika kulitafakari ikaonekana kwamba ukishatoa loophole hiyo kwa sehemu moja; na ilikuwa imeongelewa upande wa National Housing, pengine lingeweza kuleta tatizo zaidi, watu wangetumia fursa hiyo vibaya.
Mheshimiwa Spika, tunachopendekeza pengine na kuona kwamba kina unafuu zaidi, ni pale ambapo tunaweza kutumia rasilimali tulizonazo katika maeneo yetu na hasa katika kutumia hivi vifaa vya ujenzi ambavyo vinaletwa kwa karibu zaidi. Sasa hivi ukiangalia hata cement imeshuka bei kulingana na uzalishaji umekuwa mkubwa. Kadri ambavyo uzalishaji unakuwa mkubwa, ndivyo jinsi na bei inashuka.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hapa tunachohimiza ni
ile sera ya viwanda; pale ambapo tutawezesha kuwa na viwanda vingi vitakavyoweza kutengeneza vifaa vya ujenzi bei zitashuka tu kwa sababu gharama zitakuwa zimepungua na viwanda vingi vitakuwa katika maeneo ambayo usafirishaji wa vifaa vyake utakuwa ni chini. Kwa hiyo, huwezi kusema tu kwamba utapunguza hili kwa sababu watu wengine watatumia fursa hii vibaya na tusingependa itumike hivyo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunalipokea kama ni changamoto lakini pia tunahimiza kutumia rasilimali zilizopo katika maeneo yale ambapo pia ujenzi wa nyumba umeonekana kuwa ni nafuu zaidi.
Mheshimiwa Spika, hata ukiangalia katika ile Bodi ya Wakala wa Ujenzi wa Gharama Nafuu wa Nyumba ambayo iko kwenye Wizara yetu, wanatengeneza nyumba na vifaa vya ujenzi wanaandaa pale wanatengeneza, nyumba zake zinakuwa na gharama ya chini zaidi ukilinganisha na hali halisi.
Mheshimiwa Spika, swali la pili ameongelea habari
ya Sheria ya Madini kwamba unapotaka kufanya resettlement kwa watu, anatakiwa afanyiwe malipo stahiki na pia kuandaliwa makazi kwa maana ya kuwezeshwa kupata makazi mengine. Suala hili kisheria lipo isipokuwa katika utekelezaji ndiyo unakuwa kidogo haupo vizuri. Hili tumesema kwamba Serikali tutalisimamia kwa sababu ni wengi wanaoonewa katika hali hiyo.
Mheshimiwa Spika, unakuta kwamba unamuondoa katika makazi yake, unamlipa pengine stahiki yake ya fidia, lakini hukamilishi lile linalotakiwa kwamba umlipe fidia yake na bado pia aweze kupata resettlement mahali pengine. Hili tunalisisitiza kwamba lazima unapomwondoa mtu apate kiwanja aweze kujenga katika maeneo mengine, kwa sababu unalitumia eneo lile kwa uzalishaji.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tatizo kubwa ni kwamba Halmashauri zetu hazina uwezo wa kutosha wa kupima maeneo yao ili kugawa viwanja na hivyo kuwepo na makazi bora, Serikali sasa ina mpango gani mahususi wa kutoa fungu maalum kwa ajili ya Halmashauri iwe kama revolving fund, wakishapima maeneo waweze kuyauza then warudishe ile fedha na hivyo kuhamishiwa kwenye Halmashauri nyingine ili Halmashauri zote hapa nchini ziweze kupima maeneo yao na hivyo kuwa na makazi bora kwa wananchi wetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, suala alilolizungumza Mheshimiwa Sakaya, ni kweli, Halmashauri nyingi hazina uwezo wa kufanya kazi hiyo, lakini ndani ya Wizara tulikuwa tumeanzisha mfuko huu kwa ajili ya kuwezesha Halmashauri mbalimbali kuweza kupima na kuuza viwanja na baadaye kurejesha madeni yao.
Mheshimiwa Spika, lakini kumekuwa na mfano mbaya ambapo Halmashauri nyingi hazirejeshi na mpaka sasa tunadai zaidi ya Halmashauri saba ambazo zimechukua na hazijarejesha na wengine wamerejesha kiasi, na ninadhani kama Mjumbe pia anayo taarifa, tulishawasilisha wale ambao wanadaiwa.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tusingependa pia kuendeleza kuwa na madeni haya na ndiyo maana Serikali inahimiza makusanyo ya ndani ya Halmashauri zenyewe zinazohusika. Pia wanayo fursa ya kupata mikopo kutoka katika mabenki mbalimbali ambayo yanaweza kutumika katika zoezi hilo. Ndiyo maana pia tumeruhusu wataalam mbalimbali wa kutoka kwenye private sector kufanya zoezi hilo la upimaji. Katika kupima, siyo lazima ulipe cash, kuna ile barter trade tunayosema wanaweza wakafanya.
Kwa hiyo, kuna maeneo mengine ambayo wameshaanza; ukiangalia Mkoa wa Katavi, kuna maeneo mengi wanafanya kwa kukubaliana mpimaji na Halmashauri, wanaachiana asilimia kadhaa, hawalipi cash isipokuwa vile viwanja anavyopima anauza anapata hela yake na Halmashauri inaachiwa vingine kwa ajili ya kuweza kutengeneza miundombinu.
Mheshimiwa Spika, hata yule mmiliki wa kiwanja, kama ana kiwanja kikubwa kimetoa viwanja labda vitano, wanakubaliana asilimia kadhaa; anaachiwa viwanja vyake vingine wanachukua Halmashauri wanauza wanatengeneza miundombinu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, siyo lazima kuwe na cash, ni namna ambayo unaweza ukaifanya na hasa kwa maeneo ya vijijini. Kwa mijini inaweza ikawa ngumu kidogo, lakini vijijini inawezekana kwa kufanya barter trade na bado zoezi la upimaji likafanyika vizuri.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa jambo hili sasa limechukua muda mrefu tangu 2007 mpaka sasa ni zaidi ya miaka kumi na wananchi wa Enduimet na Ngarenairobi wameendelea kupata matatizo ya ardhi na maeneo ya kujenga.
Je, ni lini Serikali itakamilisha mchakato huo na kuyagawa mashamba hayo kwa wananchi hao? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa jambo hili
la ardhi pia limefanana na maeneo mengine ya Monduli na kwa kuwa Serikali iliyafuta mashamba 13 mwaka 2015 na mashamba hayo mpaka sasa pamoja na mapendekezo ya wananchi bado hayajagawanywa.
Je, ni nini kauli ya Serikali katika kuyagawa mashamba haya, iko katika mazingira gani ili wananchi waweze kunufaika nayo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la nyongeza lililoulizwa na Mbunge wa Monduli, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Waziri, ni wazi Monduli kuna mashamba mengi ambayo wameleta kwa ajili ya kufutwa na yaweze kupata umiliki mwingine, lakini mpaka sasa mashamba mengi bado yapo kwenye mchakato; zile hatua za awali zimeshafanyika lakini mpaka yaweze kugawiwa ni pale ambapo umiliki wake utakuwa umeshafutwa rasmi na kuweza kuwarejeshea ili wao waweze kupanga tena matumizi kwa ajili ya wananchi wao au kwa ajili ya uwekezaji. Kwa hiyo, hatua hiyo itakapokuwa imekamilika, watapewa na watafanya zoezi la kugawa upya kama ambavyo waliomba toka awali.
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Na mimi nilitaka kumwuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini Serikali itakuja kutatua mgogoro wa wananchi katika Kata ya Kakese katika shamba la Benki ya NBC? Shamba hili lilikuwa la uwekezaji lakini mpaka sasa shamba lile lipo limekaa dormant na wananchi hawakuweza kuendelea kulima shamba lile na shamba lile bado lina mgogoro.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri haoni kwamba
ule ni upotevu wa malighafi na wananchi wanashindwa kuendelea kuendeleza lile shamba ili waendelee kujipatia kipato?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Rhoda Kunchela, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nitoe ufafanuzi tu kwamba migogoro yote kwa ngazi tofauti siyo kwamba lazima itatuliwe na ngazi ya Wizara. Migogoro mingi na hasa ya kwenye kata na vijiji inatatuliwa na mamlaka zilizoko kule ikiwemo Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, kuna Ofisi ya Kanda ya Ardhi katika maeneo yale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu amesema mgogoro huu uko kwenye ngazi ya Kata, naomba tu Mkuu wa Wilaya wa eneo husika pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri husika waende kwenye Kata yenye mgogoro waweze kutatua mgogoro ule na wananchi waweze kupewa haki yao kama wanastahili kwa sababu amesema lilikuwa linamilikiwa na NBC, lakini siyo kila mgogoro lazima uje Wizarani.
Waheshimiwa Wabunge, nawaomba sana, migogoro mingi wakati mwingine hata tunapokwenda kufanya ziara, unakuta ni mgogoro ambao ungeweza kumalizwa na Mkuu wa Wilaya pale au Mkuu wa Mkoa au Mkurugenzi mwenyewe husika katika eneo lile. Ukienda pale unakuta wewe unakuwa kama mtazamaji, watu wanamaliza wenyewe.
Mheshimiwa Spika, nashauri tu ile ambayo inahitaji Wizara basi ijulikane na ile inayohudumiwa na Mkoa na Wilaya basi nao wachukue nafasi yao kuhakikisha kwamba wanatatua migogoro hii na isiwe ni kikwazo kwa wananachi.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongezana ninaomba kuiuliza Serikali kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imekiri kwamba hii migogoro kweli ipo na ni ya muda mrefu, Jimbo la Tabora Mjini linazungukwa na kambi nyingi za Jeshi ambazo migogoro mingi inapelekea kuhatarisha amani miongoni mwa wanajeshi pamoja na raia. Ni lini sasa Serikali au Serikali ina mpango gani wa kuwakutanisha wanajeshi wahusika ili waweze kukaa na wananchi kuweza kutatua migogoro hiyo ya ardhi iliypo Tabora Mjini?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali inafanya uhakiki mbalimbali kuanzia watumishi wa Serikali na mpaka leo tumeona wale wa vyeti, lakini ni lini Serikali itafanya uhakiki wa hawa Maafisa wa Ardhi ambao wanaingiza migogoro kwa makusudi kati ya wananchi pamoja na Serikali kwa kufanya mpango wa kugawa viwanja; kwa mfano kiwanja kimoja kutolewa zaidi ya mtu mmoja (double allocation). Maafisa hao wapo na hawajafanyiwa uhakiki ili wachukuliwe hatua. Ni lini Serikali itafanya uhakiki wa hawa maafisa wanaoleta migogoro ili na wao wachukuliwe hatua?
NAIBU WAZIRI ARDHI, NYUMBA, MAENDELEO NA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme tu ni kweli alichokisema kwamba maeneo mengi ambayo yamezungukwa na Majeshi na wala si majeshi tu hata watu wengine wa kawaida, kumekuwa na migogoro baina ya wananchi na pande ya pili inayomiliki wakiwemo Jeshi. Kuhusu zoezi alilouliza, mimi nimwambie tu kwamba naomba wananchi wa Tabora wawe na subira kwa sababu tayari zoezi la kuhakiki maeneo ambayo yana migogoro na yale ambayo yanamilikiwa na Jeshi limeshaanza. Upande wa wenzetu Wizara ya Ulinzi wameshaunda kamati ambayo imeanza kupitia katika maeneo na mimi nikiri tu wazi na ni-declare interest kwamba hata kwenye Wilaya yangu pia kulikuwa na tatizo hilo lakini tayari Kamati ile imeanza kupita na wanafanya uhakiki wa mipaka.
Mheshimiwa Spika, na wanapofika katika maeneo
yale wanahusisha uongozi wa eneo husika. Kwa hiyo, wakifika pale lazima uongozi wa Wilaya na uongozi wa Mitaa au Vijiji vinavyohusika watahusishwa ili kuweza kubaini ile mipaka iliyokuwepo toka mwanzo. Wenzetu Jeshi wameenda mbali zaidi, kwa yale maeneo ambayo watakuwa hawayahitaji baadae watasema nini cha kufanya katika eneo hilo, ikiwa ni pamoja na kuyarejesha pia kwa wananchi; lakini ni baada ya uhakiki kwasababu mengine yako strategically huwezi kuyaondoa leo na kuwapa wananchi. Kwa hiyo, uhakiki huo Mheshimiwa nikuhakikishie umeshaanza, unafanyika na Tabora watafika na tatizo litakuwa solved.
Mheshimiwa Spika, swali la pili amezungumzia suala la uhakiki wa maafisa ambao wanaingiza mgogoro kati ya Serikali na wananchi. Mimi niseme tu kwamba katika ziara ambazo tunafanya mimi pamoja na Mheshimiwa Waziri kila tunapopita tukikuta kuna tatizo hatua zinachukuliwa palepale. Ni juzi tu hapa alikuwa Lindi ambako tumekuta kuna mtu kamilikishwa eneo kubwa la wananchi zaidi ya ekari 4,000 lakini Mheshimiwa Waziri ame-declare pale pale kwamba ardhi ile irudi kwa wananchi na yule mtumishi amesimamishwa. Hata hivyo mimi pia nilipopita katika maeneo yale kuna wafanyakazi idara hiyo tumewatoa katika eneo lile na kuweza kutafuta wale wengine wanaohusika.
Mheshimiwa Spika, niseme kwa upande wa Maafisa Ardhi wale ambao ni wateule ni jukumu la Halmashauri, tukiona kwamba huyu mtu hafanyi kazi yake vizuri ni lazima tumuondoe na tunaleta jina lingine kwa maana ya ku-propose ateuliwe kuwa Afisa Ardhi Mteule; kwa sababu wale nao wasipofanya kazi yao vizuri hawa wadogo wa chini wanaharibu kazi zaidi. Kwa hiyo, ni jukumu letu sote katika maeneo yetu kuona wasiofanya kazi vizuri wachukuliwe hatua kwa sababu mamlaka ya ajira yako pale pale katika maeneo yao, kwa maana ya Mkurugenzi. (Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Mheshimiwa Spika, kuna zoezi linaendelea katika mpaka wa Tanzania na Kenya eneo la Kata za Kitendeni, Tarakea, Reha na Nanjara katika Jimbo la Rombo. Nyumba za wananchi zinawekwa ‘X’ na wameamriwa kuzivunja. Sababu wanayopewa ni kwamba wanataka kuhakiki mpaka wa Kenya na Tanzania.
Mheshimiwa Spika, nyumba hizi na wananchi hawa wameishi katika maeneo hayo kabla hata ya uhuru. Sasa naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, uko tayari kusimamisha zoezi hili ili wananchi wale wa Kikerelwa, Nayeme na maeneo mengine wapewe maelezo ya kutosha kuhusu zoezi hilo na labda pengine uko tayari tuongozane wewe na mimi kwa ajili ya kwenda kuwapa hawa wananchi maelezo ya kuridhisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunilinda.(Kicheko)
Mheshimiwa Spika, ni kweli zoezi la uhakiki katika mipaka yetu linaendelea, lakini naomba tukumbuke kwamba usalama wa nchi yetu hii tusipouangalia sisi wenyewe tunaweza tukajikuta tunaiingiza nchi katika matatizo. Kwa sababu wananchi wanapokuwa wanaingiliana katika yale maeneo ndipo hapo hapo uharifu unakuwa ni mkubwa zaidi, huwezi kujua ni nani amefanya zoezi hili.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, suala la kuhakiki mpaka tunakwenda sambamba na ile eneo ambalo ni no man’s land lazima libaki wazi, lakini pia ile buffer zone inayotakiwa kuwepo pale lazima hatua zinazotakiwa zionekane kubaki. Kwa hiyo, lazima tu katika lile eneo pawe wazi ili kuweza kutambua na kuainisha mipaka ilivyo na ile no man’s land imekaa namna gani. Na hili tatizo pia lipo hata upande wa Tunduma, Uganda na Tanzania.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi niwaombe tu kamba tunapofanya zoezi hili kama kuna mtu ambaye amevunjiwa tofauti na utaratibu pengine hakustahili kuvunjiwa hilo ndilo tunaloweza tukalisikiliza. Kwa wale waliojenga kwenye maeneo ambayo hayaruhusiwi kujengwa yanatakiwa yabaki wazi zoezi litaendelea kwa sababu ya kuangalia usalama wa nchi yetu ili tuweze kuudhibiti uingiaji holela katika maeneo. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Spika, kwanza, kwa kuwa katika Mkoa wa Dar es Salaam kuna ujenzi mkubwa unaoendelea katika barabara za Morogoro, Kilwa, Bagamoyo na Pungu, lakini Serikali inatoa hati pamoja na vibali vya ujenzi kwa wananchi hawa wanaojenga pembezoni mwa barabara. Inapotokea wakati wa upanuzi wa barabara wananchi hawa wanaambiwa kwamba wamefuata barabara na hawastahili kulipwa fidia.
Je, kwa nini sasa Serikali wanatoa vibali kwa wananchi wanajenga mpaka wanamaliza nyumba hasa nyumba ya ghorofa mpaka inaisha pasipo kutoa ushauri wa kitaalam kwa wananchi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa wananchi wanapenda maendeleo, wanajenga majumba makubwa ya ghorofa na nyumba za kawaida pembezoni mwa barabara lakini wanakosa kuelewa matumizi sahihi ya ardhi iliyopo. Je, Serikali wako tayari kutoa elimu kwenye kata, vijiji na mitaa ili kuwaeleza wananchi wetu waelewe matumizi bora ya ardhi kuingana na mipango ya maendeleo iliyopangwa na Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, la kwanza ameuliza juu ya utolewaji wa vibali katika maeneo ambayo pengine hayakustahili kupewa vibali hivyo na baadaye yanabomolewa. Naomba kupitia Bunge lako hili Tukufu nitoe wito kwa halmashauri zote; kwa sababu tuna imani kila halmashauri inazo ramani za mipango miji katika maeneo yao; na ujenzi wowote unaoendelea unaangalia ile Mipango miji yao au Master Plan ambazo zinakuwepo zinasema nini katika maeneo hayo. Hili limekuwa likifanyika maeneo mengi na Mwanza ikiwemo.
Mheshimiwa Spika, sasa niseme kwamba, katika hili na ambalo tumekuwa tukilitolea maelekezo mara kwa mara. Pale ambapo uongozi wa Halmashauri husika utatoa kibali tofauti na matumizi ya eneo ambalo limetajwa au ambapo mtu kapewa kibali kwenda kujenga, halmashauri hiyo ijue itakuwa tayari kulipa fidia hasa kwa wale ambao waliohusika katika kupeleka vibali ambavyo vinakwenda kinyume na utaratibu kwa sababu tunazo ramani na master plan zetu. Kwa hiyo, niseme hili ni jukumu la kila Halmashauri kujiridhisha kwanza kabla ya kutoa vibali vya ujenzi kwenye maeneo. Tusingependa wananchi wapate hasara kwa kujenga halafu baadaye anabomolewa.
Mheshimiwa Spika, swali la pili amezungumzia kuhusu kutoa elimu sahihi kwa wananchi ili watambue. Niseme tu kwamba, sasa hivi tuna miji zaidi ya 13 ambayo inaandaa mipango miji yake, I mean kwa maana ya kuwa na master plan. Kabla ya master plan ile kutekelezwa lazima kunakuwa na ushirikishwaji wa jamii, ukiangalia sasa hivi katika Miji ya Arusha, Dar es Salaam, Mwanza na maeneo mengine ambayo master plan zinaendelea ikiwemo na Musoma lazima kunakuwa na ushirikishwaji wa wananchi. Unapowashirikisha pale ndipo wanatakiwa na wao pia watoe mawazo yao ili kuweza kuona na watambue master plan ile inakwenda kujengeka namna gani.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi niseme elimu itaendelea kutolewa. Wizara tunavyo vipindi maalum ambavyo mara kwa mara Maafisa wetu huwa wanakwenda wanatoa na hata tunapofanya ziara tunatoa, kwa hiyo hili litaendelea kufanyika. Vile vile tuziombe, halmashauri kwa sababu unapokwenda ku- implement master plan utekelezaji wake lazima jamii iliyopo pale itambue. Pale mtu anapojenga nyumba ya kawaida wakati kwenye master plan yako inaonesha ni ghorofa, gharama ile utaibeba wewe ambaye unatoa kibali kujenga eneo ambalo tayari una Master Plan na bado unakiuka taratibu.
MHE. SALMA M. MWASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante
kwa kuniona. Sheria ya Fidia inasema kwamba watu walipwe ndani ya miezi sita, lakini katika Jiji la Dar es Salaam kwa sasa kuna uwekaji wa alama za X kwenye nyumba za wananchi usioeleweka na alama hizo zinawekwa hazina muda maalum hasa kwenye nyumba ambazo zipo pembezoni mwa barabara na maeneo mengine katika Jiji la Dar es Salaam. Unakuta alama ya X imewekwa miaka mitano, mitatu au sita; yule mwananchi haelewi hii alama ya X inakuwaje? Naomba niiulize Serikali, ni kwa nini alama ya X inapowekwa yule mtu asilipwe fidia ndani ya miezi sita awe ameshalipwa na kuondoka katika eneo lile? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ni wazi Sheria ya Ardhi kifungu namba 13(2) na (3) kinaelezea mtu unapotaka kuchukua eneo fidia ilipwe ndani ya miezi sita na kama hukulipwa ndani ya miezi sita basi kuna hali halisi ya kuweza tena kuchaji gharama hiyo kulingana na rate iliyopo katika financial institution kwa kipindi hicho. Hata hivyo, hii imekuwa haifanyiki kutokana pengine na wachukua ardhi wenyewe kutokuwa tayari kufanya ile kazi kwa wakati. Hii tumeisemea na tumeipigia kelele na ndiyo maana kukaja na ile Sheria ya Uthamini ambayo tumeifanya hapa; ambayo inazungumzia suala la baada ya miaka miwili kama mtu hajaweza kulipa fidia ule uthamini uliofanyika mwanzoni wote unakuwa umefutika. Hii ilikuwa imefanyika hivyo mwanzoni kwa sababu ile sheria ilikuwa inaachia mtu anaweza akaenda miaka 10 mpaka 20 hajalipa.
Mheshimiwa Spika, sasa tunasema baada ya kupitisha ile sheria hivi sasa ndani ya kipindi kilichotajwa lazima fidia ile ilipwe na hakuna kuchukua ardhi ya mtu kama hujalipa fidia, hili kila siku tunalirudia. Tunasema kuanzia sasa, kwa sababu wananchi wengi wameteseka katika masuala ya ulipaji fidia. Hakuna kuchukua ardhi ya mtu kama mwekezaji au yeyote anayechukua ardhi ile hajaweza kulipa fidia kwa gharama iliyopo katika soko baada ya kuwa imefanyiwa uthamini kwa kipindi hicho. Vinginevyo wananchi tunasema wasitoe maeneo yao kama hawajathibitishiwa katika kutoa eneo lile.
Mheshimiwa Spika, suala lingine katika hilo hilo, kuna shughuli zingine ambazo zinafanyika za kiserikali ambazo ukiing’ang’ania ile ardhi unakuwa umekwamisha mambo mengine. Sisi ndani ya Serikali tunajipanga vizuri kuona kwamba yale maeneo ambayo yanatumika kwa ajili ya manufaa ya umma tutayafanyia utaratibu wa haraka na mapema ili wananchi wale wasiweze kulalamika.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya shida inayowapata wanawake ni mitaji na Serikali imeweka pesa nyingi sana kwenye mabenki ili wakope, lakini wanapotaka kwenda kukopa kwenye mabenki wanaambiwa wapeleke hati, wanapokwenda kutafuta hati kwenye Ofisi za Ardhi wanahangaishwa sana; wanaambiwa wapeleke vitu vingi sana na wanaambiwa milolongo ya mambo mpaka wanaamua kuacha, zaidi ya mwaka mtu anafuatilia hati. Ni lini sasa Serikali itaweka gharama halisi za kupata hati?(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Benki ya Wanawake ipo Dar es Salaam tu, ni lini sasa Serikali itaamua kufungua matawi mengine katika mikoa mingine ili wanawake wapate huduma hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna usumbufu katika kupata hati na hasa hizi Hakimiliki za kimila ambazo tunazizungumzia kwasababu shughuli yote inafanyika katika maeneo husika na katika vijiji husika. Kwa hiyo, mimi niseme pale ambapo Halmashauri yoyote inaonekana kwamba ni kikwazo katika kuwapatia wananchi hati za Hakimiliki za kimila tuwasiliane kwa sababu lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba mwananchi wa Kijijini tunamuwezesha kuweza kupata hati yake ya Hakimiliki ya kimila.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kwasababu ndio sehemu pekee ambayo inaweza kumkomboa na mpaka sasa kama nilivyosema hati 400,761 zimeshatoka ni kwasababu tu ya ushirikiano wa karibu sana na wenyewe baada ya kuwa tumewaelimisha kwamba hati zile zinakwenda kuwakomboa katika shughuli za kimaendeleo. Kwa hiyo, pale wanapokwama naomba tuwasiliane ili tushughulikie.

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; naomba kujibu swali la pili la nyongeza la Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata na ninaomba majibu yangu yaende kwa wanawake wote wa Tanzania kwamba Benki ya Wanawake ilianzishwa kwa malengo ya kuwahudumia, lakini kwa sasa ina changamoto kubwa za kimtaji na tutafungua matawi mikoani pindi ambapo uwezo wetu wa kimtaji wa Benki ya Wanawake utakavyoimarika. Ila kwa sasa tulichokifanya ni kuhakikisha tunafungua vituo vya kuwahudumia na kuwawezesha wanawake kwenye mikoa zaidi ya 18 nchini ili kuwapa elimu ya ujasiriamali lakini pia mikopo midogo midogo isiyo na dhamana ambapo wanawake wanadhaminiana wao kwa wao. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA:Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.
Serikali ina mpango kabambe wa kupima na kurasimisha ardhi nchi nzima na imekuwa ikishirikisha sekta binafsi katika kufanya hivyo. Aidha, kumekuwa na gharama kubwa sana katika upimaji na urasimishaji huo wa ardhi. Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya mapitio ya gharama hizo ili kuweza kuwapunguzia wananchi mzigo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Zainab anazungumzia habari ya gharama kubwa katika suala zima la upimaji. Lakini naomba nimkumbushe tu bajeti ya mwaka jana ilivyosomwa gharama zile zilishuka kutoka shilingi 800,000 kwa heka mpaka shilingi 300,000 kitu ambacho ilipunguza sana gharama zinaongezeka kulingana na ukubwa wa eneo ambalo linaenda kupimwa. Kwa mwaka huu pia katika bajeti yetu nadhani kuna maeneo ambayo Serikali imeyafanyia kazi mtayasikia wakati tunatoa bajeti.
Kwa hiyo, niseme kwamba gharama tunaziangalia
na namna bora ya kuweza kumuwezesha mwananchi wa kawaida aweze kupima ardhi yake na kuweza kumiliki ili kumletea maendeleo katika shughuli zake.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwa kuwa Serikali kwa kutambua wanawake inakuwa vigumu kupata mikopo kwenye mabenki, imekuwa ikitoa hela na wakati mwingine pia ikipeleka kwenye mabenki, lakini wanawake wanakopeshwa kupitia kwenye vikundi vyao zikiwemo mabilioni ya JK.
Swali langu nauliza, wanawake wa vijijini hawakunufaika na hizo hela, sasa Serikali inafanyaje kuhakikisha kwa kuwa zile hela ni za mzunguko na bado tuna amini zipo, zitawafikiaje wale wanawake wa vijijini?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tu niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba sisi wote ni wajumbe katika zile Halmashauri zetu na mikopo inapopitishwa inapitia katika vikao vya Baraza la Madiwani.
Kwa hiyo, mimi naomba pale ambapo tunapitisha vikundi vyetu viweze kupewa mikopo ni lazima tuzingatie pia tunao akina mama wanaotoka katika maeneo ya Vijiji ili na wao waweze kufikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa suala la mabenki, benki wana masharti yao ambayo yanatakiwa yatimizwe, kwa hiyo tujaribu kuwaelimisha wakina mama ili waweze kukidhi vigezo vinavyotakiwa na mabenki na sisi wenyewe tuwe mstari wa mbele katika kuangalia ni vikundi vipi ambavyo vimekidhi vigezo hivyo na tuawasidie katika hatua za kuweza kupata mikopo either kutoka katika benki au kutoka katika Halmashauri kupitia ule Mfuko wa Wanawake na Vijana.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya asilimia 70 ya nguvu kazi ya kilimo ni wanawake, lakini ni kwa bahati mbaya sana inapokuja suala la umiliki wa ardhi, wanawake wanaomiliki ardhi ni pungufu hata ya asilimia 20. Na hata ninavyozungumza hati za kawaida na hati za kimila haziwanufaishi wanawake kwasababu sheria za nchi yetu zinatambua Sheria za Kimila ambazo zina ubaguzi.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilitaka Wizara inisaidie katika mpango wenu mpana wa kuweza kufanya maboresho kwenye sekta ya ardhi mna mikakati gani ya kuweza kuondokana na sheria kandamizi ili umiliki wa ardhi usiwe na ubaguzi hivyo shughuli za uchumi zinufaishe makundi yote? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimhakikishie Mheshimiwa kwamba sheria zetu tulizo nazo sasa pamoja na kanuni pamoja na kwamba Sera ya Ardhi pia inapitiwa upya, hazikandamizi wala hazibagui mwanamke kuweza kupata hati. Ndio maana zoezi linaloendelea sasa la kutoa hati miliki za kimila kuna mahali ambapo unakuta mke na mume wote wanakabidhiwa hati kwa pamoja, aidha wanakubaliana iandikwe jina la mke au iandikwe majina yote mawili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo tumeshaanza kuangalia kwa sababu wengi walikuwa wakinyanyasika katika hilo. Kwa hiyo, tunajaribu kupitia upya pia sera tuweze kuona lakini haya yote yanawezekana katika kufanyika ili kuweza kuhakikisha kwamba akina mama nao pia hawako nyuma katika umiliki wa ardhi. Ni kweli lilikuwepo tatizo hilo lakini limeanza kuondoka kwa taratibu.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kumalizia kazi la Mheshimiwa Mdee, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri kwamba ni kweli sheria hazibagui, lakini pia hata kama akipata mwanaume hati ya kimila au hati ya muda mrefu, wakati wowote ule mwanamke ajue ile hati ni salama. Hii ni kwa sababu kwa utaratibu wa sasa mwanaume akitaka kuuza au kubadilisha ile hati hatumkubalii mpaka tumuulize mkewe na vilevile mwanamke akitaka kuuza lazima tumuulize mumewe ili kuonyesha kwamba mali haipotei whether imeandikwa mwanaume au mwanamke wakati wa kupoteza lazima yoyote aulizwe. Kwa hiyo, mwanamke amelindwa sana katika sheria za sasa. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pia nashukuru kwa ufafanuzi alioutoa Naibu Waziri ambao utaleta mwanga kidogo kwa wananchi wa Manispaa ya Sumbawanga. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, wananchi wa Manispaa ya Sumbawanga wameamua sasa kufuata utaratibu ili wapate hati, shida yao siyo kumiliki tu hati, ziwasaidie kwenye taasisi pia za kifedha, lakini hati zimekuwa zinachelewa sana. Hamuoni kwamba kuendelea kuchelewa kwa hati hizo mnawanyima fursa wananchi wa Manispaa ya Sumbawanga na Mkoa wa Rukwa masuala ya maendeleo kwa sababu wanakosa mambo muhimu hasa katika taasisi za fedha?
Swali la pili, Maafisa Ardhi wa Manispaa ya Sumbawanga wanajitahidi sana kwa jitihada zao kuwafuata wananchi kwenda kupima maeneo, lakini wanakabiliana na changamoto za usafiri, pamoja na vitendea kazi vingine kwenda kupima ardhi.
Je, Serikali hamuoni kuna umuhimu zaidi wa kuwapa kipaumbele ili wale wakafanye kazi kwa mujibu wa sheria ili wasipate malalamiko kama yanayoendelea kwa sasa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza amezungumzia ucheleweshaji utaratibu wa kupata hizo hati pengine unakuwa ni mrefu na ni kinyume na utaratibu. Pengine Mheshimiwa Aida bado yuko na mawazo yale ya zamani, kwa sababu sasa hivi kama ambavyo tulieleza kwenye bajeti iliyopita ndani ya mwezi mmoja kama umekamilisha malipo yako vizuri, unapata hati yako, hakuna tena usumbufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kanda zetu zote Nane zinatoa hati hizo tumeishaweka wataalam kule wako wanafanya kazi hiyo. Kama huko kwake bado hilo linafanyika, nadhani siyo sahihi, na mimi siamini kama linafanyika hivyo kwa sababu utendaji wa Wizara kupitia Kanda zake unakwenda kwa utaratibu na mujibu wa sheria ambavyo tumewawekea, hivyo hakuna tena suala la ucheleweshaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Maafisa Ardhi kukosa usafiri na vitendea kazi, naomba tu nitumie fursa hii watendaji hawa ambao wako katika Halmashauri ni jukumu la Halmashauri kuweza kuona ni jinsi gani watu hawa watafanya kazi. Wizara tuna-support yale ambayo yako nje ya uwezo wa Halmashauri. Hii ni Idara kama Idara zingine, kama Idara ya Elimu, Idara ya Afya wanakuwa na usafiri, wanawekewa bajeti zao kila mnapopanga. Mnashindwa nini kufanya hilo kwa Idara ya Ardhi, kwa sababu sehemu nyingi kila unapoenda unakuta Idara ya Ardhi ile ni ombaomba, wakitaka kwenda field mpaka wabembeleze gari sijui la Elimu, lakini ni jukumu la Halmashauri husika kui-treat Idara hii sawa na Idara zingine. Kwa sababu ndiyo kwanza wanaofanya zile kazi ambazo inawezesha Idara zingine kuweza kufanya kazi zao kwa ukamilifu vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe kwamba mbali na Wizara kusaidia, ni jukumu la kila Halmashauri kuhakikisha kwamba tunapoweka bajeti zetu, katika kupanga vitendea kazi pamoja na kwamba vina gharama lakini lazima tukadirie. Wizara pia inakwenda kuweka utaratibu kwenye maeneo ya Kanda zetu kutakuwa na vifaa vya upimaji kule ambavyo vitasaidia katika Halmashauri zetu. Kwa hiyo, tusaidiane Halmashauri na Wizara ili tuwarahisishie kazi hii na wao waweze kufanya kazi zao kwa ukamilifu.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri amejibu vizuri sana, nataka niwaombe Waheshimiwa Wabunge niwape experience kidogo kwa swali la nyongeza hili kwamba hati hazitayarishwi na Wizara, hati zinatayarishwa pale kwenye Halmashauri. Sasa nawaombeni ninyi Waheshimiwa Wabunge mkirudi majumbani kwenye Halmashauri zenu mfanye tu ujanja ambao nimegundua wanafanya.
Meshimiwa Naibu Spika, nimekuta Kibaha pale hati zinaanza kuandaliwa pale Wilayani makaratasi, hata lile jalada la hati linatengenezwa pale sisi tunakuja kusaini tu huku mwisho. Mkienda kwenye Masjala za Hati kwenye Wilaya zenu zote, mtakuta hati zile zimetayarishwa ziko kwenye mafaili haziendi kokote.
Waheshimiwa Wabunge, hebu kila mmoja aende kwenye Masjala ya Ardhi ya Halmashauri yake, utakuta hati zimeshaandikiwa, watu wameshalipa wametengenezewa na yale majalada ya kaki halafu zimewekwa pale miaka miwili mitatu. Hazifiki kwa Makamishna wa Wizara ya Ardhi kusaini kwa nini? Ndiyo kazi tunayoifanya sisi wenzenu kuja kwenye Majimbo yenu kuja kuangalia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba sasa wote muwe ma-auditor muende kwanye masjala za ardhi mkaziondoe zile hati ambazo zimekaa mle, watu wanataka zikae muda mrefu wasahau halafu waweze kubadilisha wampe mtu mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, naomba mtusaidie kwenda kwenye masjala, mfanye ukaguzi watu wote ambao majalada yameshaandikwa yafike kwa Makamishna wapewe hati zao, tunataka mwezi mmoja tangu mtu amelipia apate hati yake. (Makofi)
MHE. MAFTAH A. NACHUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kabla sijauliza swali la nyongeza, naomba nifanye masahihisho kidogo. Mheshimiwa Naibu Waziri kasema eneo la Libya ni shamba la chumvi.
Mheshimiwa Spika, mgogoro huu siyo shamba la chumvi ni makazi ya watu ambao nilizungumza wakati wa bajeti hapa kwamba waliamka asubuhi wakakuta wamewekewa beacon kwamba eneo lao limeuza. Siyo shamba la chumvi. Naomba Mheshimiwa Naibu Waziri afanye masahihisho.
Mheshimiwa Spika, sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, Machi 5 mwaka huu wa 2017, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alikuwa Mtwara, pamoja na mambo mengine Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alikuwepo Mtwara Mjini na alilalamikiwa kuhusu suala la mgogoro wa ulipaji wa fidia katika maeneo ambayo yamechukuliwa mwaka 2013; Mji Mwema. Akaahidi kwamba wananchi wale watalipwa pesa zao mwishoni mwa mwezi Julai, lakini mpaka leo tunapewa taarifa kwamba yule CEO wa UTT amesema hawezi kuwalipa wale watu.
Mheshimiwa Spika, naomba kujua majibu ya Wizara hii kwamba ni kweli inawatendea wananchi hawa wa Mtwara Mjini haki? Kwa sababu tangu mwaka 2013 wamechukuliwa maeneo yao, halafu leo Serikali inasema haiwezi kulipa zile pesa. Naomba tupate ufafanuzi.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, eneo hili la Libya ambalo ni maarufu kama Mangowela, lakini wale waliochukua lile eneo kwa kuwanyang’anya wananchi eti wanawaeleza wawahamishe, wamebatiza jina wakaita Libya, lakini asili yake ni Mangowela. Sasa naomba kujua, yule mtu ambaye amewanyang’anya wananchi wale ni taasisi inaitwa Azimio na Serikali imemchukulia hatua maeneo mengi. Je, Serikali iko tayari hivi sasa kumnyang’anya ardhi ile ambayo ameidhulumu kwa wananchi na badala yake wananchi wale wameambiwa waende Mahakamani wakati wanajua kabisa kwamba anafanya ujanja kule Mahakamani? Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme tu nilikuwepo huko mwezi uliopita na bahati nzuri nilionana na uongozi wa mkoa pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mtwara- Mikindani.
Mheshimiwa Spika, sasa wale kama wameshindwa kulipa au wameshindwa kuchukua, hatuwezi kuendelea kuwalazimisha kwa sababu ile ardhi ni mali. Kama wameshindwa, maana yake ni kwamba mnunuzi yeyote ambaye anataka kuwekeza pale, anaruhusiwa kuja. Wale wamesha-declare kwamba hawawezi na hatuwezi kuwalazimisha. Kama wame-declare hawawezi, maana yake ni kwamba tunaangalia utaratibu mwingine na hili liko chini ya Mkuu wa Mkoa analisimamia.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Wizara yangu inasubiri wao wenyewe wahusika kwa maana ya Manispaa pamoja na Mkoa husika kwamba watakuja na mpango upi au watakuja na utaratibu upi ambao watakuwa wamejiwekea? Kwa maana ya UTT, hawawezi tena na wamesha-declare kwamba hawawezi kuchukua.
Mheshimiwa Spika, suala la pili analolizungumzia, lipo Mahakamani na siwezi kulijadili hapa na ndiyo maana nimetaja na namba ya shauri lilipo Mahakamani. Tusubiri shauri hilo liishe ndiyo waweze kulileta hapa.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Swali la kwanza, kwa kuwa jibu la msingi la Serikali inakiri kwamba shamba hili lilipata hati kuanzia mwaka 1978 mpaka mwaka 1981.
Je, ni kwa nini Serikali haikuwa na hati ambayo leo hii mwekezaji huyu amekuwa akiwaonea wananchi wa vijiji hivyo tajwa alivyovitaja Mheshimiwa Waziri?
Swali la pili, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbarali akiwemo na Mkuu wa Wilaya ya Mbarali binafsi siwaamini katika utekelezaji wao wa kazi zao. Je, Mheshimwa Waziri huoni umuhimu wa mimi na wewe kuongozana na kwenda kuwasikilisha wananchi na wanakijiji wa Nyelegete waliokataa kusikiliza mahusiano yao, mimi na wewe tukaenda kwa pamoja. Ni lini na utakuwa tayari tukaongozana kwenda kusimamia hili?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza anasema ni kwa nini Serikali haikuwa na hati. Si kweli kwamba Serikali haikuwa na hati kama anavyosema, maeneo yote yanayomilikiwa na Serikali yanafahamika toka awali, na wanakijiji wanaozunguka eneo lile walitambua kwamba lile lilikuwa ni eneo la Serikali.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, suala la kumuuzia mmiliki mwingine tofauti na Serikali ili aweze kuishi vizuri na wanakijiji wanaomzunguka ni lazima ule uhakiki wa mipaka ufanyike kwa kuhusisha pande zote ambazo zinahusika katika mgogoro huo, kwa sababu huwezi ukampa tu wakati huo huo na wananchi pia nao walikuwa wanalitazama shamba lile.
Mheshimiwa Spika, lazima kufanya ule uhakiki wa mipaka ili kumfanya huyu mwekezaji ambaye yupo aweze kutambua mipaka yake vizuri. Kwa vyovyote unavyouza kwa mtu lazima umkabidhi eneo lako na kuhusisha kwamba ni wapi ambapo mipaka yako inaishia. Kwa hiyo, suala hilo nadhani linaeleweka kwa staili hiyo.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anasema habari ya kwenda Mbarali, nakumbuka mwezi Machi nilikwenda katika Mkoa wa Mbeya na Mbarali nilifika na suala hili lilizungumzwa, lakini kama bado halijatatuliwa na mgogoro bado upo, nadhani tutaangalia ratiba itakavyokuwa imekaa ili tuweze kuongozana na kusikiliza wale wananchi jinsi wanavyolalamika lakini najua chini ya mikono salama ya Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi masuala hayo yatatatuliwa. (Makofi)
MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, wananchi wapatao 200 wa Makambako Kata ya Kivavi, Mtaa wa Mashujaa waliondolewa katika maeneo yao mwaka1997 bila kupewa fidia, kwa ajili ya kupisha ujenzi wa soko la kimataifa, wamefuatilia wananchi hawa lakini hadi leo hakuna majibu. Pia kuna wananchi wa Idofi waliondolewa maeneo yao kwa ajili ya kupisha ujenzi wa mizani hadi leo hawajapata fidia.
Je, Serikali inampanga gani wa kuwalipa wananchi hawa fidia zao?
Swali la pili, kwa kuwa kila Halmashauri kuna Maafisa Mipango Miji. Je, ni kwa nini wananchi wanajenga sehemu zisizo sahihi na Serikali inawaangalia tu mwisho wa siku wanaanza bomoa bomoa? Naomba kupata majibu (Makofi).
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na sehemu yake ya kwanza wananchi 200 wa Makambako na wale wa Kidozi kwamba walipisha miradi ya Serikali na mpaka leo hawajalipwa fidia. Naomba nimhakikishie tu Mheshimiwa Mlowe kwamba mara pesa zitapopatikana watalipwa, kwa sababu Serikali inatambua kwamba ililitwaa lile eneo kwa ajili ya matumizi ya Serikali, kwa hiyo, asiwe na wasiwasi pesa ikipatikana watalipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili anaongelea habari ya maafisa kwamba watu wanajenga ovyo na wanaangalia na hakuna hatua zinazochukuliwa baadae wanakuja kuwabomolea. Naomba nitoe rai tu kwa sababu pia ni sehemu ya Halmashauri na tunakaa katika vikao vyetu vya Halmashauri kwa maana ya Baraza la Madiwani, haya yanapotokea ni wajibu wetu pia kutoa maonyo kwa wale ambao wamepewa wajibu huo wa kufanya kazi lakini hawasimamii sawasawa. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Mbunge atakapokuwa amekaa katika Baraza lake la Madiwani wajaribu kuwakumbusha hasa wale watendaji ambao hawatimizi wajibu wao vizuri.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza.
Pamoja na kazi nzuri na jitihada za Serikali katika kuhakikisha miji inapangwa na zoezi zima la urasimishaji wa makazi ikiwemo upimaji shirikishi, naomba tu kujua Serikali inayo mkakati gani kuhakikisha kwamba pamoja na upimaji huu unaofanyika sasa ile gharama ya premium inaonekana kuwa mzigo mkubwa kwa wananchi na matokeo yake wanashindwa kufikia hatua ya kupewa hati miliki, hivyo inawapelekea kubaki katika maeneo ambayo yamepimwa bila hati hizo.
Je, ni nini mkakati wa Serikali kuondoa kabisa hizi asilimia 2.5 zilizopunguzwa japo ilikuwa Saba ikapunguzwa, nini mkakati wa Serikali kuondoa hizi lakini kuongeza muda wa upimaji shirikishi ili wananchi wengi zaidi waweze kupimiwa kuhakikisha maeneo yao yote yamekamilika? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Bunge hili Tukufu kwanza naomba nimshukuru Mheshimiwa Mabula kwa sababu jana pia wakati anachangia Mpango wa Maendeleo amezungumzia suala la kuwajali sana wananchi na hasa katika suala zima la urasimishaji na mpango unaoendelea. Ametupa changamoto kama Wizara na sisi tunamshukuru na tumeona iko haja kweli ya kuangalia hawa wananchi ambao walitumia nguvu zao kujenga katika maeneo ambayo pengine hatukuwa makini katika kuwahi kupanga na wao wakavamia, basi tumesema kwa sababu hoja ni kupunguziwa mzigo, tumelichukua suala lake kuondoa premium na kabla ya mwisho wa mwezi huu tutakuwa tumempa jibu.
Je, ni lini zoezi hili litaendelea, naomba nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa maeneo yale ambayo yanarasimishwa na yamekwishaanza kwa mwaka huu tutavumilia mpaka mwisho wa mwaka huu wa fedha. Baada ya mwaka wa fedha tuna imani na mipango miji katika maeneo hayo, mipango kabambe katika maeneo hayo itakuwa tayari kwahiyo ukomo wao itakuwa ni mwisho wa mwaka wa fedha mwaka huu 2017/2018.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Angelina mwenzangu, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Swali la kwanza, kwa kuwa Mheshimiwa naibu Waziri amekiri kuwa wananchi wanavamia na kuyamega maeneo ya Serikali kinyume na utaratibu; na kwa kuwa ametoa rai wananchi waondoke maeneo hayo kabla sheria haijachukua mkondo wake, sasa isije ikawa kwa wananchi kilio, kwa watendaji vigelegele.
Je, Serikali ina kauli gani juu ya watendaji ambao wanalipwa mshahara kwa kazi ya upimaji na katika maeneo yao hawajafanya lolote hadi sasa?
Swali la pili, kwa kuwa katika majibu ya msingi, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema gharama elekezi za huduma ya upimaji siyo kubwa kama inavyoonekana au inavyodhaniwa.
Je, kwa nini gharama hizo zisiwekwe wazi ili wananchi na taasisi nyingine wafahamu na kuzitambua na waweze kujipanga kwa ajili ya kulipia? Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali la kwanza ameulizia habari ya adhabu kwa watendaji ambao wanafanya makosa na tunaadhibu pengine wananchi. Kama nilivyomjibu muulizaji wa swali namba 44 majukumu na uwajibishaji yako chini ya mamlaka husika hasa katika maeneo yetu kwenye Halmashauri za Wilaya. Kwa hiyo, haya yanapobainika basi tuyachukulie hatua papo hapo ili tusiweze kuwafanya wananchi waumie zaidi kwa makosa ya watendaji wetu.
Swali la pili, ametaka kuewekewa gharama za upimaji wazi. Naomba niseme tu tutazitoa na tutawagawia Waheshimiwa Wabunge wote, lakini kwa kifupi tu nikianza kuzungumzia habari ya miji kwenye Mamlaka za Miji na Manispaa katika gharama za upimaji kuanzia square meter moja mpaka square meter 400 gharama yake kwa maeneo ya residential ni shilingi 65 lakini maeneo ya commercial ni shilingi 350 kwa square meter, kwenye industrial ni shilingi 450 na kwenye maeneo ya social services ni shilingi 150. Kwa miji yetu ya kwaida kwenye township ni shilingi 200 kwa makazi, maeneo ya biashara ni shilingi 300, maeneo ya viwanda 350 na maeneo ya services ni shilingi 100. Vivyo hivyo kwenye trading center ni shilingi 100 kwa makazi, shilingi 200 kwa commercial, shilingi 200 tena kwa industrial na shilingi 100 kwa services. Kwa sababu mlolongo pia unategemeana na ukubwa wa kiwanja vina-range kuanzia shilingi 300,000 mpaka milioni 14 kutegemeana na ukubwa kuanzia hekari moja mpaka 10 ni shilingi milioni tatu, zinakwenda zinaongezeka kadri ya ukubwa, tutaziandaa na tutawasambazia Waheshimiwa Wabunge wote.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kuuliza swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya asilimia 56 mpaka 60 ya watanzania ni vijana lakini vijana wanashindwa kutimiza malengo yao ama ndoto zao kutokana na gharama kubwa ya upangaji wa nyumba za makazi hasa mijini kuwa kubwa na wamiliki kutaka kupewa kodi za mwaka au miezi sita.
Je, ni lini sasa Serikali itafuta utaratibu huu na sisi kama Bunge tutunge sheria itakayowalazimisha wamiliki wote kupokea kodi ya kila mwezi badala ya mwaka ama miezi sita kama ilivyo sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimpongeze kwa kuona kwamba ipo haja ya kuona kwamba wapangaji wa nyumba wanakuwa na sheria ambayo inasimamia katika suala zima la upangaji. Naomba nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge pamoja na Wabunge kwamba Wizara tayari imekwishaliona hilo na tayari tupo kwenye mchakato wa kuanzisha mamlaka itakayosimamia masuala yote ya nyumba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika sheria hiyo ambayo italetwa hapa Bungeni, tumeangalia suala zima la ukomo wa kutoa kodi za nyumba, hiyo ya miezi sita na mwaka mmoja haitakuwepo kwa sababu tumeona inaumiza watu wengi. Kwa hiyo, kodi itakuwa inalipwa kwa mwezi mmoja mmoja na wakati huo huo utatakiwa kuweka kama amana ya miezi mitatu kwa ajili ya shughuli ambazo zinaweza kuwa, kwa hiyo nimesikia na tunalifanyia kazi. (Makofi)
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Tabora Manispaa imeathirika sana na migogoro ya ardhi. Kuna kata ambazo zinapakana na maeneo ya jeshi, ambazo ni Kata za Cheyo, Mbugani, Tambuka Reli, Uyui na Micha. Maeneo yale yamekuwa na migogoro ya mipaka ya muda mrefu. Je, Wizara ya Ardhi imejipangaje kwa kushirikiana na Wizara ya Ulinzi ili waweze kuoanisha sasa mipaka halisi ili kuweza kutatua migogoro hii ya mipaka katika kata hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Tabora kama nilivyosema manispaa imekuwa na migogoro mikubwa ya ardhi na hasa bomoa bomoa. Tabora imeathiriwa sana na zoezi la bomoa bomoa; si maeneo ya reli tu lakini hata maeneo mengine yanayopaka na mashule kama Tabora Girls…
Wananchi wale na maafisa kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri wengine si waaminifu. Je, Serikali kwa kuwa hawa wananchi wengi waliobomolewa hayakuwa makosa yao, inawachukulia hatua gani hawa ambao wamesababisha wananchi wamepata hasara kubwa na sasa hawana hata amani na wamekuwa katika hali isiyoeleweka?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza amezungumza habari ya mipaka kuathiri maeneo yaliyopakana na Jeshi na ametaja kata ya Cheyo, Tambuka Reli na nyingine. Naomba tu nimthibitishie Mheshimiwa Mwakasaka kwamba Wizara ya Ulinzi ilishachukua hatua ya kuunda Kamati ambayo imepitia katika maeneo yote ambayo yana migogoro ya Jeshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo hayo walikuwa wakifika wanaongea na watu wa eneo lile na kuweza kubainisha mipaka; kwa sababu kuna mengine ambayo wananchi lakini maeneo mengine Jeshi liliingia ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kabla ya kuanza kuweka mipaka upya au kuipitia kwanza wanachambua yale maeneo. Wakishamaliza shughuli hiyo ndiyo Wizara itaingilia kati katika suala la kupanga. Hata hivyo, kwanza tuitambue tuibaini ili kuondoa ile migogoro. Zoezi limeshaanza katika baadhi ya wilaya na Kamati ile inafanya kazi vizuri kwa sababu inashirikisha uongozi wa maeneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la bomoa bomoa katika maeneo ambayo yamevamiwa au watu wamebomolewa pengine hawakuwa na tahadhari; kwanza naomba nitoe tahadhari kwa wananchi wengi, kwamba maeneo mengi ya taasisi za umma yamevamiwa sana na wananchi na wengine wamejenga nyumba za kudumu kwa muda mrefu. Hata hivyo, unapoangalia kisheria na taratibu na ukubwa wa shule yanayotakiwa kuwa unakuta sehemu nyingi yamevamiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa makosa ya watendaji wetu kuna wengine pia walithubutu kutoa hati katika maeneo ambayo ni ya shule. Kwa hiyo zoezi hili linafanyika ili kuhakikisha kwamba maeneo yote yanapimwa na yanatambulika na wale wote walioingia ndani basi sheria inachukua mkondo, wake kwa maana ikiwa ni pamoja na kuvunjiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wale ambao watakuwa wamevunjiwa kimakosa ni lazima uhakiki ufanyike tuweze kujua pengine hata ile hati aliyonayo si sahihi. Kwa hiyo kama tukikuta mtu amevunjiwa katika utaratibu ambao ni wa kimakosa basi tutaona namna ya kuweza kumpatia kiwanja mbadala. Nitoe rai tu kwamba wale wote walioko kwenye maeneo ya umma ni vizuri wakayaachia.
kwa kunipatia fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imeanzisha utaratibu mzuri wa kuwashirikisha Wenyeviti wa Serikali za Mitaa kwa kuwapatia ramani za maeneo husika, je, Serikali itaweza kwenda mbali zaidi na kuwajengea uwezo pamoja na kuwapatia elimu Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Madiwani ili waweze kusimamia maeneo yale ya wazi na ujenzi holela?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Hivi karibuni Serikali imeweka zuio katika Mkoa wa Dar es Salaam kwa watu ambao wamejihamasisha kubadilisha mashamba yao na kupima viwanja ili waweze kujenga na kuuza. Kwa sababu Serikali yenyewe imeshindwa ama kwa kiasi kikubwa haina uwezo wa kukidhi mahitaji ya ujenzi wa viwanja kwa ajili ya wananchi, haioni sasa ni muda muafaka kuweka utaratibu wa jinsi ya kupata kodi badala ya kuweka zuio?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile katika swali lake la kwanza ameishukuru Serikali kwa kutoa ramani kwa Wenyeviti wa Mitaa ili kuweza kulinda na kuhifadhi maeneo yao lakini akataka kujua kama Serikali haioni kwamba kuna haja ya kuwajengea uwezo. Naomba niseme tu kwamba swali lake ni la msingi sana na kama nilivyokuwa naeleza muda mfupi uliopita, watu hawa wanahitaji pia kupewa elimu ya kutosha kuweza kutambua ramani zile na namna ya kuzisimamia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu Wizara imeonyesha dhamira ya dhati kutaka kulinda maeneo ili yasivamiwe kwa kushirikisha elekezi kwa sababau tumeona maeneo kama Kigamboni kuna makampuni zaidi ya matano yamepima maeneo yale lakini kila kampuni ina bei yake ya kiwanja. Kuna wanaouza square meter moja shilingi 25,000/=, kuna wanaouza shilingi 20,000/= na kuna wanaouza kwa shilingi 10,000/=. Ni nani Mtanzania wa kawaida ataweza kununua? Serikali pia huwa inapima lakini gharama zake hazijafikia hata shilingi 10,000/= kwa square meter moja, iweje wao wapime na kuuza katika bei kubwa za namna hiyo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Serikali imeamua kwa maana ya Wizara kusitisha kwanza zoezi hili na wiki hii bei elekezi itakuwa imeshakamilika na itatoka ili viwanja hivi hata kama wanapima, tunashukuru kwa sababu wanasaidia katika kupanga miji yetu, lakini wapange miji na kuweza kuuza viwanja katika bei ambayo mlaji wa kawaida ataweza kumudu, isiwe ni bei ambazo zinakwenda kubeba wale watu wenye pesa na wasio na pesa watajikuta hawana viwanja. Kwa hiyo, dhamira ya Serikali ni njema na naomba Waheshimiwa Wabunge mtuunge mkono na wiki hii bei elekezi itatoka na viwanja vitaendelea kupimwa kama kawaida lakini kwa maelekezo mazuri ya Wizara. wahusika wenyewe, niwaombe Halmashauri husika kwa sababu Wenyeviti hawa sio wengi sana kwa kushirikiana na Wizara yangu waweze kuweka utaratibu mzuri ili watu hawa waweze kupewa angalau ABCs za kuweza kusoma na kutambua ramani zile ili waweze kufanya kazi yao kwa ufasaha zaidi. Maana tukishawawezesha hawa, kwa sababu pia siyo wote wanaofurahia namna ambavyo miji yao inaharibika, wengi wanachukia, watakuwa katika position nzuri ya kuweza kusimamia jukumu ambalo wamepewa sasa ambalo linastahili kusimamiwa katika maeneo yao. Kwa hiyo, niseme tu Wizara yangu itashirikiana na Halmashauri kuandaa mipango mizuri ili watu hawa waweze kupewa elimu ili waweze kusimamia vizuri maeneo yao kama ambavyo wameelekezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili amezungumzia habari ya zuio la Wizara kwa upimaji unaoendelea katika maeneo mbalimbali. Nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge watambue kwamba hatua iliyochukuliwa na Wizara ina lengo zuri na hasa la kutaka kuwalinda walaji wa kawaida kwa maana watu wa kawaida ambao wanatafuta viwanja kwa ajili ya kuweza kupata maeneo yao. Sheria ya Mipangomiji Na. 8 ya mwaka 2007 inaruhusu watu binafsi kupima maeneo hayo lakini kwa kuzingatia taratibu za maeneo hayo.
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri amesema katika jibu lake hapa kwamba Halmashauri zijitahidi kuweza kuwapa semina au mafunzo Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Maafisa wengine. Hata hivyo, Wizara yake inadaiwa na Halmashauri, kwa mfano, Halmashauri ya Manispaa ya Temeke tunadai gawiwo la asilimia 30 ya shilingi bilioni moja kutokana na gawiwo la kodi ya ardhi. Tangu mwaka 2014 tunadai na tunauliza hawatujibu, hawaoni kwamba juhudi za Halmashauri kuweza kupanga, kutoa elimu zinakwamishwa na Wizara yenyewe kwa kutokurejesha ile asilimia 30?
Makazi, majibu mafupi.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nimesema hapa kwamba Halmashauri zishiriki katika suala zima la kuwajengea uwezo Wenyeviti hawa lakini kwa kushirikiana pia na Wizara. Maana ya kujenga uwezo ni kwa kutumia mapato ya ndani ya Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la asilimia 30 kutorudi kwenye Halmashauri, naomba niseme tu kwamba, tunapokusanya mapato haya, yanakwenda kwenye kapu moja la Serikali ambapo tunakwenda kugawana keki wote kwa pamoja na pale pesa hizo zinaporudi Wizarani mara moja zinakwenda katika maeneo husika. Tunatambua wazi kwamba Halmashauri nyingi zinadai lakini katika kudai pia kuna Halmashauri nyingi pia Wizara inazidai ambazo walikopeshwa pesa kwa ajili ya kupima viwanja. Kwa hiyo, pesa wakati mwingine inapoingia Wizara inakata katika kufidia madeni ambayo imetoa ili pesa ile iweze ku-generate na kuweza kuwapa Halmashauri nyingine lakini Halmashauri nyingi zaidi zinadai.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwahakikishie tu kwamba tumekwishachukua takwimu sahihi za madai yanayodaiwa kwa asilimia 30. Kwa hiyo, mara tutakapopokea fedha kutoka Hazina na sisi tutazituma moja kwa moja. Nia na dhamira ya Serikali ni nzuri ya kuweza kuhakikisha mpango unakwenda vizuri kwa kushirikisha pande zote. Kwa hiyo, zitakapokuja hizi fedha tutazileta na tunajua zitasaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tahadhari pia, tuna malalamiko likiwepo lalamiko kutoka Halmashauri ya Magu kwamba pesa hizi zikirudi Wakurugenzi wanazipangia shughuli nyingine na idara husika haipewi. Kwa hiyo, tuseme pesa hizi zikirudi kule zinatakiwa zirudi kwenye idara husika ili zifanye shughuli ya utawala wa ardhi na siyo kuzipangia matumizi mengine. Naomba sana Wakurugenzi ambao wanazitumia ndivyo sivyo, basi tunakwenda kufanya uhakiki ili tuweze kuona ni namna gani pesa hizi zitafanya kazi iliyokusudiwa.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Ni lini Wizara itakuja Wilaya ya Mkalama kutugawia ramani mpya Wabunge na viongozi husika na kutuonyesha mipaka ya Wilaya kwa Wilaya ili kuepusha migogoro inayoendelea sasa na inayosababisha uvunjifu wa amani kama ambavyo imejitokeza katika Jiji la Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimwa Allan ametaka kujua ni lini Wizara itagawa ramani kama ilivyofanya Dar es Salaam ili kuweza kuepusha uvamizi katika maeneo hayo? Naomba nirudie tena kusema kwamba zoezi hili limefanywa na Wizara kwa kuanzia Dar es Salaam lakini lengo la kufanya kwa kila Mkoa na kila Halmashauri inao wajibu wa kutoa ramani hizi kwa Wenyeviti wake ili waweze kulinda maeneo yao siyo kwamba Wizara itakwenda katika kila Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nirudie tena kusema kupitia katika Bunge lako hili kwamba Halmashauri zote zinatakiwa kusimamia zoezi hili na hasa katika maeneo ambayo migogoro imekuwa mingi katika maeneo ya mjini ambapo viwanja vimevamiwa ovyo ovyo ili waweze kuona ni jinsi gani wataweza kutawanya ramani hizo ili watu waweze kulinda maeneo yao. Kama kuna tatizo pengine katika uelimishaji wa kusoma zile ramani basi Wizara inaweza ikasaidia kutoa wataalam kwenda kushirikiana na Halmashauri kuwafanya hawa watu waweze kusoma ramani vizuri na kuweza kuyalinda maeneo yao. Kwa hiyo, nizitake tu Halmashauri ziweze kufanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, anasema ni lini tutakwenda kwa ajili ya kubainisha mipaka ambayo ipo…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, swali la nyongeza lazima liwe moja, kama yalikuwa mawili, basi umeshamaliza kujibu hilo moja. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Ndiyo Mheshimiwa Naibu Spika.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.
Mheshimiwa Spika, japo nia ya Serikali ni njema kurasimisha ardhi kwenye maeneo ambayo hayajapimwa,
lakini kuna concern kwamba tunakuwa tunaendeleza squatters, maeneo ya wazi ambapo miundombinu inakuja
kuwa challenge. Sasa badaye mnapotaka ku-implement mambo ya mipango miji au ramani zetu tulizonazo kutakuwa kuna gharama tena husika za kubomolea watu. Je, Serikali nimezingatia hili? Asante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli anachozungumza nadhani kama nimejibu vizuri, ulinisikiliza wakati najibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Allan, si nia ya Serikali kuona kwamba miji inaendelea kuharibika kwa kuendeleza squatter na ndiyo maana nimewaomba Waheshimiwa Wabunge kwa sababu wote ni Wajumbe wa Baraza la Madiwani katika Halmashauri zetu, pale ambapo Serikali imeanza kufanya zoezi la urasimishaji katika maeneo ni jukumu la kila Halmashauri kuhakikisha kwamba wanasimamia maeneo yao ili kusiwe na muendelezo wa ujenzi holela. Kwa sababu zoezi hili linapaswa kusimamiwa na Halmashauri zenyewe husika, Wizara sio rahisi kushuka kila maeneo.
Mheshimiwa Spika, ni kweli zoezi tunalifanya na inaonekana ni zuri, lakini tusingependa kuona ujenzi holela
unaendelezwa. Sasa ujenzi huu utasimama pale ambapo kila halmashauri itawajibika katika eneo lake kuhakikisha inakuwa na michoro ya mipango miji kwenye maeneo yao na kusimamia zoezi la ujenzi holela lisiendelee katika maeneo yao. Tukifanya hivyo, miji yetu itakuwa salama na itakuwa inapendeza.
MHE. MAULID S. A. MTULIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza.
Mimi katika maeneo yangu ya Jimbo langu la Kinondoni, hasa Magomeni Mtaa wa Kwa Suna, Hananasifu
Mtaa wa Mkunguni na mitaa mingine, nyumba za wananchi zilifanyiwa urasimishaji, lakini kwa masikitiko makubwa watu wakatumia fursa ile wengine kwenda kukopa. Nasikitika kwamba Serikali imeenda kuvunja nyumba zile bila kulipa fidia kwa wananchi wale.
Je, kwa nini Serikali inavunja nyumba zilizofanyiwa urasimishaji na kupata leseni za makazi bila kulipa fidia?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, anachokizungumza ni kweli, kuna maeneo yalifanyika hivyo, lakini suala la msingi hapa kupewa leseni ya makazi haina maana ya kwamba pale ambapo utaratibu wa mipango miji umeyapanga vinginevyo yale maeneo hautavunjiwa. Kwa sababu Dar es Salaam yenyewe sasa hivi iko katika mchakato na ninadhani imekamilisha mpango wa master plan ya mji ule.
Sasa pale ambapo inaonekana kabisa kwamba kuna suala zima la kutaka kuweka miundombinu inayofaa katika
eneo lile watu hawa wanaweza kuvunjiwa katika maeneo yao.
Mheshimiwa Spika, lakini Wizara ilishatoa tangazo kwa wale ambao walikuwa na umiliki halali na wana hati
kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na wamevunjiwa kimakosa, tulisema walete orodha yao na watu wa mipango miji watakwenda kuhakiki waone kweli walivunjiwa kimakosa. Lakini kwa wale ambao waliendelea na ujenzi bila kuzingatia mipango miji imepanga nini katika ule mji hao hawatalipwa na itakuwa ni tatizo. Watu wa Hananasifu na Mkunguni kama alivyosema, kama hao wapo kulingana na maelezo niliyoyatoa, basi tupate wakiwa na hati zao kutoka Wizarani kwetu au kutoka kwenye ma nispaa inayohusika, tutawa-consider kulingana na malalamiko watakavyokuwa wameyaleta.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuweza kunipatia nafasi ya kuuliza swali.
Kufuatia majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, je, ni lini Wizara itashuka chini kwenye Halmashauri mpya kama
vile Mkalama, ikarasimisha maeneo ya wananchi kwa sababu kuna miji midogo inayochipua ambapo wananchi wanahitaji maeneo yao yarasimishwe ili waweze kupata mikopo na ardhi yao iwe na thamani?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, mimi ningependa kushauri halmashauri mpya zinazoanzishwa, tusikimbilie kwenye suala la urasimishaji, kwa sababu urasimishaji si suluhu ya kupanga miji yetu. Mimi ninachomshauri Mheshimiwa waingie katika maandalizi ya kuwa na mpango kabambe wa kupanga mji wao, ili miji hii yote mipya inayoanza ianze katika mpangilio mzuri wa mipango miji na si kuanza zoezi la kurasimisha. Lakini kwa maeneo ambayo tayari yameshaendelezwa bila kufuata taratibu za mipango miji tutakuwa tayari kushiriki pamoja nao katika kuhakikisha kwamba tunafanya zoezi la urasimishaji, lakini wakati huo huo waingie katika mpango wa maandalisi ya mpango kabambe.
MHE. SALMA M. MWASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza naishukuru Serikali kwa kutambua umuhimu wa urasimishaji, lakini naomba itekeleze kwa vitendo.
Mheshimiwa Spika, ili kupunguza migogoro ya ardhi suluhisho muhimu ni kupima, kupanga na kurasimisha na si
vinginevyo. Kumekuwa na miradi ya urasimishaji, kwa mfano mradi unaondelea sasa hivi katika Jiji la Dar es Salaam Kimara, mradi ule ni kama umetelekezwa. Wafanyakazi wale hawana hela za kwenda site, hawana mafuta na wala hawana vitendea kazi vyovyote katika.
Mheshimiwa Spika, kama hivi ndivyo sasa tuone kwamba kurasimisha inakuwa ni sehemu ya kufanya thamani
za ardhi zile kupanda hasa katika Jiji la Dar es Salaam ambako squatter sasa hivi katika Jiji la hilo ni tatizo kubwa.
Watu wanajenga hovyo, mji unachafuka, haupangwi inavyostahili.
Mheshimiwa Spika, sasa huu mradi uliokuwa pilot area kwa ajili ya Dar es Salaam ambao sasa ungeweza
kufanya huko kwenye mikoa mingine. Sasa ni kwa nini Serikali haipeleki fedha kwenye mradi ule na kutoutelekeza kama ilivyo sasa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali namba la pili, katika miradi ile ya MKURABITA kwenye urasimishaji huo huo, wananchi
walilipa fedha zao huko huko Kimara, wamelipa kati ya shilingi 400,000 mpaka 800,000. Wananchi wale bado wana zile risiti, sasa je, napenda Wizara inahakikishie ni lini hizo hela zitarudishwa kwa wananchi au kuwarasimishia ili waweze kuondokana na hiyo sintofahamu?
Mheshimiwa Spika, je, ni lini Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa tayari kuongozana na mimi kwenda katika hiyo ofisi ya mradi hapo Kimara tuangalie hayo matatizo na mimi kama mtaalamu nimshauri?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Mwassa kwa kufuatilia, lakini vilevile Mheshimiwa Mwassa ni mmoja wa Wajumbe wa Kamati yetu ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Amekuwa ni mstari wa mbele katika shughuli hizi na pia ni mwanataaluma hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niseme kwamba kwa maswali yake mawili aliyoyauliza habari ya kutopeleka fedha
katika mradi wa Kimara si kweli. Naomba nisema zoezi la urasimishaji linaloendelea Kimara halijakwama kwa ajili ya pesa, limekwama kwa ajili ya wananchi wengine kutotoa ushirikiano; na hii inatakiwa pia Halmashauri zote kule ambako zoezi hili linafanyika tuwasihi wananchi wetu watoe ushirikiano.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu suala la urasimishaji si la mtaalamu kwenda pale na kuamua nini kifanyike.
Anapokwenda katika eneo la mradi ni lazima ashirikishe viongozi waliopo lakini pia wale ambao wanapaka katika
yale maeneo yanayofanyiwa urasimishaji. Ikitokea mmojawapo akagoma au akakataa kukubaliana na kile
ambacho kinafanyika zoezi haliwezi kuendelea. Kwa hiyo, mimi niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge tuwasihi
wananchi wetu kwa sababu zoezi hili lina manufaa kwao na kwa nchi pia.
Mheshimiwa Spika, swali la pili amezungumzia habari ya MKURABITA, kuhusu habari ya kurudishiwa pesa.
Mheshimiwa Spika, miradi yote iliyoanzishwa na MKURABITA bado inaendelea kufanyika na hii ni kwa sababu
tu, kumekuwa na miradi mingi ambayo inaendelea katika maeneo ambapo baadaye MKURABITA walisimama
wenyewe, ikiwepo na ile Kusini, walisimama hawakuendelea na hilo zoezi kutokana na tatizo kama hilo hilo la mwanzo ambalo nimelizungumzia.
Mheshimiwa Spika, lakini kwa wale waliolipa pesa zao hakuna atakayedhulumiwa na wote tutawatambua. Kwa
hiyo mimi naomba kama unayo orodha, kwa sababu pale ofisini kwetu hatujawa na orodha, hatujaletewa malalamiko hayo kwa maandishi na kujua kwamba kuna watu wamechangia lakini hawajapewa huduma hiyo. Kwa hiyo mimi nitamwomba Mheshimiwa Mbunge alete orodha hiyo, na Waheshimiwa Wabunge wengine kama kwao kuna watu wenye madai hayo wayalete na ofisi itakuwa tayari kuyashughulikia.
MHE. LUCY S. MAGERELI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri sana inayofanywa na Wizara ya Ardhi lakini bado uhitaji wa suala hili la uandaaji ramani ningeendelea kupendekeza kwamba lifanywe na Wizara ya Ardhi badala kurudishwa kwa Halmashauri kwa sababu bado Halmashauri zetu zina mbinyo mkubwa sana wa bajeti.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuandaa mipango maalum kupitia Wizara ya Ardhi kuhakikisha kwamba ramani za Mipango Miji ya jumla kwa maana ya master plan zinapatikana nchi nzima na kuacha zile detailed plan ndiyo zifanywe na Halmashauri?
Swali la pili, kwa maelezo ya Mheshimiwa Waziri anasema kwamba ameacha Halmashauri zishirikiane na sekta binafsi kwa ajili ya kuandaa hizi ramani za Mipango Miji. Sitaki kukubaliana na ningependa nieleze tu bayana kwamba katika kuliachia Halmashauri zetu suala hili linafungulia mianya ya rushwa na wananchi wengine kushindwa kumudu gharama, kwa sababu sasa hivi ukipeleka mchoro wako binafsi au kuomba mchoro binafsi unaambiwa wewe mwenyewe ndiyo uugharamie mpaka na kikao cha Halmashauri kikae kwa gharama ya mwombaji kupimiwa eneo la ardhi. Je, Serikali haioni kwamba inafungua mianya rushwa na kuwafanya wananchi washindwe kabisa kupata huduma hii kwa ufanisi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme tu kwamba nakubaliana naye katika swali lake jinsi alivyouliza, kwa sababu taratibu zinazoendelea mpaka sasa suala zima la upangaji miji ni jukumu la Halmashauri zenyewe. Napingana naye kwenye suala la kusema kwamba Wizara ifanye kazi hii. Wizara kazi yetu ni kusimamia sera na tunaposimamia sera maana yake tunafanya ufuatiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tukumbuke mwaka 2016 Waziri alitoa ramani kama kuleta chachu kwenye Halmashauri zetu zote ili waweze kufanya jukumu hilo ambalo ni la kwao kama mamlaka za upangaji miji. Mara nyingi kama wananchi kule na hasa kwenye maeneo ya vijiji Wenyeviti wa Mitaa kama hawatambui maeneo yao migogoro inakuwa mingi. Kwa hiyo, nitoe rai tu kwa Halmashauri kuendelea kutekeleza jukumu lao la kuandaa zile ramani na baadaye kuzishusha mpaka kwenye maeneo ya vijiji na mitaa kule ili wale wenye dhamana kule waweze kuchukua jukumu lao la kuelimisha watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika zoezi linaloendelea la urasimishaji kwa mujibu wa Ilani ya Uchaguzi Ibara ya 37 (d)(4) ambapo urasimishaji unaendelea, bado zoezi la kugawa linatakiwa liendelee katika utaratibu huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Mbunge akubaliane kwamba Wizara haiwezi kupora mamlaka ya Halmashauri isipokuwa tutaendelea kuwakumbusha ili watimize wajibu wao. (Makofi)
MHE. JULIUS K. LAZIER: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijauliza swali la nyongeza naomba nikiri kwamba kwa kweli naipongeza Wizara hii kwa jitihada kubwa ambazo imefanya katika kusaidia wananchi wa Wilaya ya Monduli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kabla pia sijauliza swali la nyongeza, naomba nimwambie tu Waziri kwamba waliokuandalia majibu wamekudanganya. Kwanza kwa mujibu wa taarifa tu ekari zilizofutwa Monduli ni ekari 13,000 na si 131,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, mashamba tunayoyazungumzia ni mashamba ambayo Mheshimiwa Waziri wa Ardhi alivyokuja katika Jimbo la Monduli mwaka 2016 mwezi Machi, alizuiliwa na wananchi njiani na akatoa maelekezo kwamba Halmashauri ifanye mchakato wa mashamba yale ambayo yalikuwa na mashamba pori na wananchi wale walikuwa wanasumbuliwa na wale ambao waliyatelekeza mashamba na kuchukua mikopo kwa hati ya mashamba yale. Waziri akatoa maelekezo ambayo ndiyo ambayo mchakato wake ukafanyika na tarehe 09 Januari, 2018 tuka-submit taarifa ya Wilaya kwa kamishina wa ardhi wa kanda ambae taarifa yake haionekani hapa, kwa hiyo mchakato wa Halmashauri tulishamaliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri, nataka nijue tu kwamba, kwa kuwa jambo hili Waziri wa Ardhi alishatoa maelekezo na kwa kuwa Halmashauri ilishafanya mchakato wa kuyafuta mashamba haya 25, je, ni lini Serikali itamalizia huu mchakato wa ufutaji wa mashamba hayo 25 ambayo tumeanza mchakato upya kama ulivyoeleza?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Waziri alitoa pia maelekezo kwamba mapendekezo ya matumizi ya mashamba yale 13 yaletwe na kwa kuwa Halmashauri na wananchi tumeshamaliza mchakato wa kutenga maeneo kwa ajili yauwekezaji, maeneo ya akiba ya ardhi na maeneo mengine ya wananchi na kwa kuwa huu ni msimu wa kilimo na mchakato huo bado haujakamilika japo Halmashauri imeshakamilisha na taarifa yote iko Kanda; ni lini Serikali itaagiza Mkoa na Kanda walete mapendekezo ya wananchi ya matumizi ya mashamba hayo 13? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anataka kujua ni lini mchakato utakamilika. Mchakato wa kukamilika unategemea na wao wenyewe kwa sababu si kazi ya Wizara kufuatilia na kuweza kujua ni jinsi gani mchakato unakwenda mbele; kwa hiyo wao wameshaona hawajaendelezwa na sheria zipo. Ibara ya 45 mpaka ya 47 kuna maonyo ambayo yanaweza kutolewa kwa muhusika kama hajaendeleza; na Ibara ya 48 unabatilisha kwa maana ya kumpelekea ilani kwa ajili ya ubatilisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wao wenyewe ndiyo wanatakiwa wakamilishe na wakileta kwa Waziri haina tatizo. Kwa hiyo si jukumu la Wizara kuona ni lini itakamilishwa ni mchakato ambao unatakiwa umalizwe na Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili anauliza kwamba ni lini Wizara itaagiza Mkoa ili waweze kutimiza. Kila Mkoa unataratibu zake katika mipango yake, kwa hiyo kama mlileta maombi mahitaji ambayo mnataka kutumia yale maeneo ni jukumu lenu pia kuona kwamba maeneo hayo yanatakiwa yafanyiwe kazi ile iliyokusudiwa. Kwa sababu unapoleta kubatilisha tayari umeshaona kuna hitaji na tayari una mpango.
Mhe shimiwa Mwenyekiti, kwenye jibu langu la msingi nimesema kwamba hawajaleta mpango wowote kwa hiyo sisi hatuwezi kuwasukuma mfanye nini pengine hamjahitaji kwa maana hiyo. Kwa hiyo, ni jukumu la Mkoa kuhakikisha taratibu zote zinakamilika na Wizara inaweza ukafanya pale ambapo itakuwa imeletewa ofisini.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mweyekiti, nampongeza sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini kwa sababu Mheshimiwa Mbunge anasema kazi zote ziko kwenye kanda na watumishi wa kanda ni wa Wizara sisi tutafuatilia kule kwenye kanda tuone yale yaliyokwama yaje haraka Wizarani ili niweze kuyaona. (Makofi)
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nilikuwa na mambo mawili. Kwanza ni swali na pili ni ushauri.
Mheshimiwa Mwenyekii, ni kweli kabisa watalaam walikuja Muheza na walikwenda wakaangalia hiyo sehemu na Wana Muheza waliahamasika sana baada ya kuwaona watalaam hao. Hata hivyo tangu watalaam hao wamendoka nafikiri mwezi mmoja au miwli iliyopita bado hawajarudi. Sasa nilitaka kujua, ni lini watalaam hao watarudi tena na ujenzi wa hizi nyumba utaanza?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili ambalo naona kama ni ushauri; ni kwamba eneo ambalo linajengwa ni eneo la Chatur sehemu ya Kibanda, Kata ya Kilulu na lina ekari 83. Sasa nyumba ambazo zimeshawekeana saini ni nyumba 20, kwa hiyo ina maana kwamba kuna eneo kubwa ambalo litabaki. Ni ushauri tu kwamba ni kwa nini sasa hivi Shirika la Nyumba lisianze marketing kushawishi wana Muheza waanze kulipia kwenye hizo nyumba ambazo zitajengwa ili eneo lote la ekari 83 liweze kutumika ipasavyo? Pamoja na hayo, ni vizuri wakati marketing hiyo inafanyika basi na watu wa benki wanakuwepo ili kuweza kutoa mikopo kwa wananchi wa Muheza. Nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anauliza ni lini watalaam hawa watarudi tena na ujenzi uanze kuanza. Naomba nimwambie tu kwamba tatizo ambalo limefanya wasianze mapema ni kwa sababu mpango wa matumizi ya eneo lile awali watu wa Muheza walipanga kama eneo la matumizi ya umma, kwa maana walikuwa wamekusudia kuweka stand pale. Sasa unapobadilisha kupeleka kwenye kujenga makazi inabidi mchakato wa kubadili matumizi ya eneo lile ufanyike. Kinachofanyika sasa ni kubatilisha ili litoke kwenye matumizi ya umma na liende kwenye eneo la makazi, wakikamilisha wataanza kazi hiyo.
Swali la pili, anasema marketing ianze kufanyika kwa ajili ya zile nyumba 10 ziweze kununuliwa. Napenda nimhakikishie tu Mheshimiwa Balozi Adadi kwamba tayari wanunuzi wameshaanza kujitokeza, wanachosubiri ni kuona nini kinafanyika pale. Kwa wazo lake la kusema mabenki wasogee nadhani hilo tunalichukua na ni kawaida ya National Housing wanafanyakazi sambamba na mabenki katika zoezi zima la uendelezaji miliki.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nataka kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu ya kuridhisha.
Lakini kwa niaba ya wananchi wa Dar es Salaam na hasa wa hili eneo la Kawe, huu mgogoro ni wa muda mrefu sana. Kama ambavyo Naibu Waziri anasema anataka kushirikisha sasa jamii kuona namna ya kuwapa fidia wale wamiliki wa mwanzo mimi naomba kwamba ushughulikiaji wa suala hili Mheshimiwa Naibu Waziri bado ni mdogo sana. Sasa nataka tu nipate majibu ya uhakika kwamba Mheshimiwa Naibu Wziri unawahakikishia nini watu wa Kawe juu ya upatikanaji wa ardhi ili waweze kuondokana na adha hii ya upatikanaji wa ardhi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tatizo hili la migogoro ya ardhi Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana hii alishawahi kutuletea taarifa Wabunge hapa Bungeni kwamba tuorodheshe migogoro mingi kwenye majimbo yetu, lakini asilimia kubwa ya migogoro ile bado haijashughulikiwa, nini kauli ya Serikali juu ya kushughulikia migogoro ya ardhi nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ameuliza tunawahakikishia nini wananchi hawa ili kuwapa maeneo mengine waweze kuwa na makazi. Nadhani kwenye jibu la msingi nimeeleza wazi, kwa sababu eneo lile walilivamia na kulikuwa na mashauri mahakamani na bado wananchi wale wakaonekana ni wavamizi. Hata hivyo kwa busara ya Serikali, kwa sababu tulishaona eneo lile limevamiwa kwa kiasi kikubwa, Wizara ikaamua kuwarasimishia, kwa hiyo walitakiwa kurasimishiwa ili waendelee kuwepo pale na wamiliki maeneo yale, lakini wale wananchi hawako tayari kurasimishiwa. Na tukumbuke eneo lile kisheria si la kwao, ni wavamizi na mahakama ilishatamka.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama wao hawatakuwa tayari kwa zoezi ambalo Serikali imetaka kuwasaidia ili warasimishwe pale basi utaratibu mwingine Serikali haitasita kuchukua kwa sababu mahakama ilishatoa maamuzi na Serikali imeona iwasaidie kwa kuwarasimishia na wao wakae pale kihalali. Kwa hiyo, hatutakuwa na mpango mwingine nje ya pale waliponapo, kwa hiyo kama ni maeneo mengine itabidi wagharamie wenyewe kwenda kununua na waweze ku-settle kama ambavyo tunatoa viwanja kwa watu wengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili anaongelea habari ya migogoro; ni kweli tuliorodhesha migogoro mingi na iliundwa Kamati ya Wizara zaidi ya tano na migogoro ile imekuwa ikishughulikiwa katika kila Wizara na migogoro ambayo ilikuwa inaelekea kule, lakini tayari kuna ushauri ambapo kuna kamati iliundwa kwa ajili ya kutoa ushauri wa namna ya kuwa na ufumbuzi wa kudumu wa migogoro ile na tayari Kamati ile ilishamaliza kazi yake, italetwa mtaona namna ambavyo tunakwenda kushughulikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa migogoro mingine yote ambayo ilikuwa ndani ya uwezo wa Wizara husika, moja wapo ikiwa ni Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Kilimo, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Maliasili na Utalii; wote tumeshiriki pamoja na wenzetu ambao walikuwa wameandaliwa kufanya kazi hiyo.
Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Wizara inafanyia kazi na muda si mrefu mtapata ufumbuzi wa kudumu ambao umepangwa kwa ajili ya kuondokana na migogoro hiyo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nashukuru kwamba, Wizara inatambua kwamba Mji wa Tarime unatakiwa kupimwa, lakini pia inatambua kwamba una upungufu wa watumishi. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa maeneo mengi ya Mji wa Tarime yalikwishaandaliwa ramani ya Mipango Miji, lakini mpaka sasa hivi hayajapimwa, na kwa kuwa wananchi wanaendelea kujenga kiholela na kuharibu ramani ambayo tulikwishaandaa hapo awali, ni kwa nini sasa Serikali msiweze kuunda kikosi kazi kwa ajili tu ya kuja kupima maeneo yote ambayo yameshaandaliwa ramani ya mipango miji ili sasa tusiharibu hii ramani ambayo imeshaandaliwa?
Swali la pili, kwa kuwa Halmashauri ya Mji wa Tarime haina vifaa vya kuweza kupima ardhi na tumekuwa tukikodi kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Musoma, na kwa kuwa, Halmashauri ya Mji wa Tarime hatuna fedha za kuweza kununua vifaa hivi ambavyo vinauzwa bei ghali sana, ni kwa nini sasa Serikali isiweze kufadhili ununuzi wa vifaa hivi ili kuweza kupima maeneo mengi zaidi na kuweza kuharakisha umilikishaji wa ardhi kwa wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anasema maeneo mengi ya Tarime yalikuwa yamepimwa, yana michoro tayari, lakini upimaji wake pengine haujakamilika na yameanza kuvamiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali hilo naomba nijibu kwamba kwanza niwaombe Halmashauri yenyewe husika kwa sababu ndio kwanza inazidi kukua sasa hivi, kama maeneo yale hayajakamilika katika upimaji niombe Halmashauri iwe makini katika kulinda yale maeneo yasivamiwe, kwa sababu katika maeneo yote yenye michoro wananchi wanapovamia, hapatakuwa na upimaji mpya. Maana yake wakikutwa wamevamia kiwanja kimoja watu wawili/watatu, maana yake pale lazima mmoja itabidi apishe apewe kile kiwanja na mwingine atafutiwe eneo lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufanya lile eneo lisiingiliwe na watu wengi zaidi niwaombe sana Halmashauri kwanza wakamilishe ile taratibu kwa sababu ni jukumu pia la Halmashauri, lakini watasaidiwa pia na Ofisi yetu ya Kanda ambayo sasa hivi wamesogezewa, itakuwa iko Simiyu. Kwa hiyo, tukishafanya hivyo tutakuwa tumelinda yale maeneo. Urasimishaji unaofanyika hauwezi kufanyika katika yale maeneo ambayo tayari yalikuwa yamepimwa, unafanyika katika maeneo ambayo yapo katika ule utaratibu upo.
Kwa hiyo, suala la kuwa na vikosi kazi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, kazi hii inafanyika haraka ni jukumu pia la Kanda husika kwa sababu, tunaweza tukatumia Wataalam walioko katika Halmashauri jirani wakiratibiwa na Ofisi ya Kanda, suala hilo linaweza likafanyika na inawezekana kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la vifaa; suala hili nilishalijibu pia katika majibu ya nyuma katika Bunge hili. Niombe sana Wizara haiwezi kununua vifaa vya upimaji katika Halmashauri zote, ni jukumu la kila Halmashauri kuweka bajeti zake, Wizara imejipanga katika Kanda zake na vifaa vile katika Kanda vinaweza kutumika katika Halmashauri yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wazi vifaa vile vina bei kubwa sana, lakini ninaomba na nimekuwa nikielekeza wale wenzetu walioko kwenye Kanda, kila mmoja ana Halmashauri zake ni kiasi cha kupanga utaratibu mzuri, mkiwa na vikosi kazi ambavyo vinaweza vikasaidia katika kwenda Halmashauri moja baada ya nyingine itaturahisishia katika kupunguza kero ya upimaji.
Kwa hiyo, naomba pamoja na private sector ambao wanatumika, bado Ofisi zetu za Kanda kwa kutumia watumishi katika Halmashauri kwenye Mkoa husika tunaweza tukapunguza tatizo hilo. (Makofi)
MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Huu ni ubunifu mkubwa na wa kupongezwa kwa wananchi wa Manyoni Mashariki kwamba tuwe na eneo sasa litambuliwe la katikati ya nchi, na kwa sababu taarifa za awali zinaonyesha kwamba eneo hili liko kwenye Manyoni Mashariki. Nina maswali mawili ya nyongeza.
(a) Kwa kuwa Serikali imeona umuhimu wa kulitambua, kulipima na kulitangaza eneo la katikati ya nchi kwa lengo la kukuza utalii; na kwa kuwa wananchi wa Manyoni wako tayari kushirikiana na Serikali katika kuliendeleza eneo hilo pamoja na kujenga mnara mrefu ambao utawekwa taa au bendera ya Taifa.
Je, Waziri anaweza kutoa maelekezo sasa hivi hapa ndani amuagize Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani aanze kazi hiyo mara moja ya kulitambua eneo hili? (Makofi)
(b) Kwa kuwa lengo kubwa hapa ni kukuza utalii na kuongeza vivutio vya watalii, tunayo hazina ya mali kale, kubwa eneo la Kilimatinde pale Manyoni.
Je, Waziri na Maliasili na Utalii atakuwa tayari kufuatana na Mbunge kwenda kuona eneo hilo ambalo ni hazina kubwa ya kumbukumbu za biashara ya utumwa pamoja na ngome za wakoloni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza amesema je, niko tayari pengine kutoa tamko hapa, ili Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani aende aanze kufanya kazi hiyo; nadhani katika jibu langu la msingi nimesema kwamba Wizara sasa tayari inaweka mikakati ya kuweza kufanya ufatiliaji wa karibu, kwa sababu tumeona kuwa na eneo ambalo linatambulika kama ndilo center (katikati) ya nchi si tu kwamba tutatambua eneo hilo na kuliacha kama lilivyo, lakini bado ni sehemu ambayo inaweza ikatumika pia kama utalii. Ndiyo maana nimesema uendelezaji wa eneo hilo, unaweza ukafanyika katika mustakabali wa kutaka patambulike.
Mheshimiwa Spika, na kwa sababu wananchi wa Manyoni Mashariki wanasema wako tayari kushirikiana mara zoezi hilo litakapoanza tutawashirikisha kwa pamoja ili tuweze kuona suala lile linafanyika katika umakini zaidi ili kuweza kupafanya pawe kivutio cha kweli.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake la pili la kuweza kutambua vivutio vilivyoko katika maeneo ya Kilimatinde, nadhani hili ni la Wizara ya Utalii, lakini kwa sababu wote tunajenga taifa moja, tutashirikiana na wenzetu kuweze kuona maeneo hayo yanatambulika na yanaingia katika historia, lakini pia kuweka kama vivutio vya utalii ili paweze kufikika pia na patakuza soko la utalii kwa nchi yetu.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII:
Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Manyoni.
Mheshimiwa Spika, Mbunge wa Manyoni tunamshukuru sana kwa kutupa taarifa ya malikale hizo ambazo ziko katika eneo hilo na ninataka nimhakikishie kwamba tuko tayari kutembelea eneo hilo na kufanyia kazi vivutio hivyo, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Jiji la Mbeya halina master plan, general plan scheme na limekuwa katika data collection ya almost bilioni1.5. Swali langu ni kwamba je, Serikali haioni kwamba sasa ni wakati muafaka wa ku-push hili jambo lifike mwisho?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Waziri walishatembelea katika Jiji la Mbeya na nilikuwa bega kwa bega, mguu kwa mguu na Mheshimiwa Naibu Waziri yeye mwenyewe amejionea ni jinsi gani Jiji la Mbeya limekuwa ni la squatter kwa muda mrefu sana, hususan katika maeneo ya Isanga, Ilemi, Nzovwe, Iyunga, Kalobe, Nonde, Mwakibete, Sinde, Soweto; yote haya na mengineyo mengi ni Squatter kwa muda mrefu sana. Swali langu kwa Serikali, haioni kuwa sasa ni wakati muafaka tena wa kusaidia up grading katika maeneo hayo? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI:Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mwanjelwa kwa sababu mara nyingi katika Bunge hili kama tutakumbuka kila akileta swali la Makazi mara nyingi anapenda kutolea mfano wa Mbeya ambao unakuwa pengine haujawa na master plan mpaka dakika hii, lakini ni mji ambao unakuwa kwa kasi kubwa. Sasa hivi Wizara yangu inayo miji karibu 28 ambayo tayari michakato yake ya master plan inaendelea.
Mheshimiwa Spika, Jiji la Mbeya bado halijawa, mimi niwaombe sana watu wa Mbeya tuanze maandalizi ya kuwa na master plan kwa sababu mchakato mzima lazima uanzie kwenye eneo husika. Ni wazi kama wataanzisha kama ambavyo miji mingine imeanza kama Arusha, Dar es Salaam na Mwanza ambayo imeishaanza, sasa mimi niseme tu kwamba Jiji la Mbeya nalo sasa linatakiwa lianze mchakato huo kwa sababu ni suala ambalo litafanya libadilishe kabisa mandhari ya mji wenyewe.
Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la pili, ni kweli nikiri kwamba nilikwenda Mbeya na tuliongozana naye, na maeneo anayoyataja ni kweli hayavutii kwa kasi ya namna ambavyo ilivyo. Mimi nimpongeze kwa sababu pia, amekuwa na kiu ya kutaka kuona mabadiliko yanakuwepo.
Mheshimiwa Mwanjelwa naomba nikuhakikishie kwamba kwenye maeneo ya Iyunga, Kalobe, Uyoe, Nonde, Mwakibete, Sinde, Isanga, Soweto na kadhalika, kweli nilijionea maeneo hayako katika hali nzuri.
Mheshimiwa Spika, sasa mimi niseme pale ambapo mtaanza master plan, basi tutawekeza pia katika maeneo hayo kuhakikisha kwamba yanabadilika ikiwa ni pamoja na kubadili mandhari kama ambavyo ulivyoomba kuweza kufanya ile pulling ya land kuweza kuleta pamoja na kuweza kujenga majengo ambayo pengine yatapendeza zaidi au kuweka mandhari ambazo zitafanya ule mji kweli uonekane kweli ni Jiji.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ukiangalia majibu ya Mheshimiwa Waziri amesema kwamba waliokopeshwa kwa kutumia hatimiliki za kimila takribani ni shilingi bilioni 59, lakini ukiangalia idadi ya wanaomiliki hati hizo miliki za kijiji wako wengi, sasa hii inaonesha kwamba kuna tatizo katika wakopeshaji.
Sasa je, Waziri atakubali kulifuatilia jambo hili ili kuhakikisha kwamba wale wanyonge ambao hasa ndiyo wanalengwa kwa sasa wanapata mikopo bila usumbufu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Sheria Namba Nne na Namba Tano ya mwaka 1999 ya Ardhi ya Vijiji iko wazi na inatakiwa marekebisho kwa sababu wanaokwenda kutoa haki inapotokea matatizo ya ardhi vijijini ni mabaraza ya kata. Lakini kwa kuwa kuna tatizo pale.
Je, Waziri atakuwa tayari kukutana na Waziri wa TAMISEMI na yeye Waziri wa Ardhi ili kurekebisha kwa sababu haki haitendeki kama ambavyo inatakikana?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anasema imeonekana ni wazi kwamba wahitaji wa mikopo ni wengi, lakini wanaokopeshwa ni wachache. Hapa kuna mambo mawili kuna either watu kuogopa kwenda kuchukua mikopo au benki kutokubali zile hatimiliki za kimila.
Napenda nimthibitishie tu kwa sababu elimu inayotolewa wanapopewa zile hati za haki miliki za kimila wanaambiwa zina sifa sawa sawa na hati zingine na ndiyo maana benki 11 zimeweza kutoa hizo shilingi bilioni tisa na ninawapongeza sana watu wa Mbozi ambao ndiyo wanaongoza kwa kutoa mikopo kwa kutumia hati miliki za kimila. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa swali lake la pili ambalo amelizungumzia naomba tu niseme kwamba kweli tunayo changamoto hiyo na hasa ya uelewa, kwa maana katika maeneo mengi tunahitaji kuwa na watu ambao ni waajiriwa wanaoweza kufanya kazi hiyo ya kusimamia Mabaraza ya Ardhi. Sasa kama hilo linaonekana ni tatizo nadhani bado tunaweza tukaliangalia. Ni kweli kuna shida na maeneo mengi Mabaraza ya Ardhi ya Kata hayafanyi kazi yake vizuri pengine kutokana uelewa mdogo au kutokuwa na manpower ya kutosha, kwa hiyo, hili tunalichukua tutalifanyia kazi.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu yanayoridhisha ya Mheshimiwa Waziri, mgogoro huu, kama mwenyewe anavyokiri ni wa muda mrefu na mimi nimeshakwenda kwa Mheshimiwa Waziri wa Ardhi akaniambia kwamba mgogoro huu bado uko kwenye ngazi ya mkoa, watakaposhindwa ngazi ya mkoa watauleta Wizarani. Nimekwenda kwa Mkuu wa Mkoa ameniambia kwamba yeye ameshauandikia Wizarani kwa maana ya kwamba wameshashindwa.
Mheshimiwa Spika, hata h ivyo, mimi mwenyewe binafsi nimemuandikia Mheshimiwa Waziri kumjulisha mgogoro huu mpaka sasa hivi sijapata majibu yoyote. Sasa kutokana na huu mkanganyiko wa kauli za Serikali, Mkuu wa Mkoa anasema hili na Waziri anasema lingine, nini kauli ya Serikali juu ya mgogoro huu yaani nani kati yao yuko sahihi?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, anasema mgogoro huu utashughulikiwa mwaka huu wa 2018/2019. Je, Mheshimiwa Waziri, yuko tayari kuandamana na mimi baada ya Mkutano huu twende akaangalie hali halisi? Kwa sababu tayari watu walishaanza kuchomeana ufuta, juzi hapa ufuta wa Kijiji cha Mirui umekatwa na wananachi wa kutoka Kilwa.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya familia, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa namna ambavyo wameshiriki katika msiba huu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni wiki mbili tu kabla ya msiba nilikuwa kule na nimefika mpaka kwenye jimbo lake. Taarifa nilizozipokea kutoka mkoani, walisema migogoro yote walikuwa wameorodhesha na wakasema kama mkoa wameunda timu za kiwilaya wanashughulikia migogoro yao, itakapowashinda wataileta Wizarani na taarifa ya maandishi wamenipa.
Mheshimiwa Spika, nataka tu nimhakikishie kwamba pamoja na kwamba timu ya Wizara iko kule katika kushughulikia ule mgogoro, lakini pia mkoa ulijiridhisha na ukaniridhisha pia mimi nilipokuwa kule kwamba migogoro yao wanaisimamia wenyewe kwa sababu haijawashinda na wakikamilisha Wizara itakwenda kuweka mipaka, hasa katika yale maeneo ambayo yana utata wa mipaka.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii. Kama ilivyo Liwale, Wilaya ya Hanang kila upande imezungukwa na migogoro ya mipaka kati yake na Mbulu, Singida na Kondoa. Nataka kujua TAMISEMI itachukua hatua gani, kwa sababu imekuwa muda mrefu mno, hatimaye watu watauana kule ili haya matatizo ya mpaka yanayotukabili yaweze kutatuliwa na watu waishi kwa amani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Migogoro ya mipaka iko mingi katika maeneo mengi lakini suluhisho la kwanza katika kutatua ile migogoro ni kwa pande zote mbili za maeneo husika kukaa. Kwa hiyo, pale wanapokuwa wamekaa wamekubaliana kwa pande zote mbili na hasa panapokuwa na utata, hapo ndipo Wizara inakuja kuingia kwa ajili ya kusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe tu, pamoja na swali la Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu na wengine ambao wana migogoro, pale inaposhindikana ndipo hapo tunatakiwa kuingilia kati kwa sababu huwezi kuingilia kati kabla pande zote mbili hazijakaa na kuridhia na kwa kuangalia zile GN zilizounda maeneo hayo ziko katika utaratibu upi.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza swali langu halijajibiwa. Niliuliza kwa nini Serikali haisemi ukweli ndani ya Bunge? Kwa sababu hapa nina Hansard mbili Serikali ikiahidi kulipa fidia wananchi hawa, lakini pia kuna maelezo ambayo siyo sahihi sana kwenye maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, Serikali hii ya Awamu ya Tano inafanya mambo makubwa sana, imeweza kununua ndege, imeweza kuwa na mkakati wa kujenga standard gauge, lakini pia imeweza kuweka mkakati wa kujenga Stiegler’s Gorge, inashindwaje kulipa fidia ya shilingi bilioni nane kwa wananchi wa Jimbo la Mtwara Mjini maeneo ya Mjimwema? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naomba kujua, katika kuilazimisha Halmashauri sasa kuwaeleza wananchi waweze kupimiwa viwanja, wapo wananchi waliokubali na wengine hawajakubali. Je, kwa kuwa hili suala la Taasisi ya UTT-PID ipo ya chini ya Serikali Kuu, Serikali iko tayari hivi sasa kuja Mtwara Mjini na kuweza kutoa elimu kwa wananchi hao wa Mjimwema na Tangira ili waweze kukubaliana na maamuzi ya Serikali? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa kutokana na swali lake jinsi alivyouliza, majibu ya Serikali ni sahihi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, alitaka kujua kwa nini Serikali haisemi ukweli Bungeni juu ya fidia ya wananchi wa Mtwara? Na sisi tumeongelea habari ya fidia aliyoitaka ya UTT. Mpaka sasa hivi anavyozungumza UTT haidaiwi kulipa fidia yoyote kwa wananchi wale kwa sababu tayari Manispaa imeshachukua mradi ule na zoezi limeshaanza na wananchi wanapimiwa na kuna makubaliano ambayo wameingia kati ya wananchi na Manispaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kule hakuna anayedai fidia, kwa maana hiyo, kwa sababu tayari baada ya UTT kujitoa wananchi kupitia Halmashauri yao wameamua kuchukua eneo lile na kuanza kupimiwa na viwanja wanapewa kama sheria inavyosema. Kwa hiyo, Serikali imejibu kulingana na swali lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili analotaka habari ya kutoa elimu, sisi tuko tayari wakati wowote tunatoa elimu, tuna vipindi mbalimbali na hata wakitaka twende kule tutakwenda kwa sababu ndiyo kazi yetu kuelimisha wananchi ili waweze kuelewa haki zao za msingi na waweze kufanya mambo yao pasipo kubughudhiwa.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri maswali mawili madogo ya nyongeza.
Kwa kuwa kitendo hicho cha kuwachukliwa ardhi wananchi sio kitendo chema, je, Serikali haioni kwamba wananchi hao tayari imewatumbukiza katika dimbwila umaskini?
Swali la pili, kwa kuwa mwananchi huyo ameridhia zoezi la kuchukuliwa ardhi yake pasina ridhaa yake, je, kwa nini Serikali isingelitoa sehemu mbadala ili kuondoa manung’uniko kwa wananchi hao kuona wameporwa ardhi yao?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anasema kitendo cha kutwaa maeneo ya wananchi pasipo ridhaa yao ni kwamba ni kuwaingiza katika umaskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, Sheria ina ruhusu eneo likishatangazwa kuwa ni eneo la upangaji miji, Mamlaka za Upangaji kisheria zimeruhusiwa kuyatoa yale maeneo. Hiyo ni alternative ambayo iko kisheria, lakini katika hali halisi ambayo inaendelea sasa na kwenye kanuni ambazo zipo tumesema kwamba unapotaka kutwaa ardhi ya mtu, wananchi wanapaswa kushirikishwa. Kwa hiyo, kile kitendo cha kutwaa ardhi bado sheria inawaruhusu Mamlaka za Upangaji kuitoa ile ardhi na kupanga kile wanachoona inafaa katika utaratibu huo.
Sasa tunasema tunayo hiyo room ya kufanya makubaliano au maelewano na wananchi, lakini Serikali inapotaka kufanya jambo na eneo limeshaanishwa hauwezi tena wewe mwananchi kuzuia shughuli za Serikali zisifanyike. Sasa katika ule utoaji ndio hapa sasa tunasema hekima na busara pia itumike katika kuwaelimisha wale wananchi ili waweze kuelewa lengo na nia njema ya Serikali ni nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili anaongelea habari ya kwamba Serikali kwamba kwa nini isitoe maeneo mengine ambayo bado hayajaendelezwa ili kuondokana na taratibu hizi. Sasa labda nitoe tu rai kwa Mamlaka za Upangaji Miji. Kwa sababu suala la upangaji miji ni suala ambalo liko chini ya Halmashauri zetu. Kwa hiyo kwa vyovyote vile wanapoandaa mipango yao ile ni master plan waangalie utaratibu mzima namna ya kuukuza ule mji ili uweze kwenda vizuri kutegemeana na mahitaji ya wakati huo. Lakini kikubwa kinachofanyika pale ushirikishwaji hata kama utatwaa eneo ambalo ni la wananchi ni yale makubaliano kwa mfano kama umepanga hapani eneo la biashara au la huduma za jamii maana yake mwananchi atapaswa kupisha. Kama ni biashara mpe nafasi yeye ya kwanza kama anaweza kuendeleza yeye mwenyewe apewe kipaumbele badala ya kumuondoa na kuleta mtu mwingine mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na hilo tumekuwa tukilisema sana kwa sababu imekuwa ni kelele, watu wanalalamika. Kwa hiyo narudia kusema pale mnapopanga matumizi ya maeneo yenu, mnapoweka mikakati ya mipango kabambe, lazima mwananchi aliyepo afikiriwe mwanzo kama ni viwanda basi kama yeye ataweza ajenge, hawezi atauza lakini mmilikishe na umpe masharti kwamba hili ni eneo la viwanda utapaswa kujenga kiwanda, hawezi ataingia ubia, hawezi atauza ataondoka.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi kwanza niipongeze Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya chini ya Waziri mwenye dhamana Naibu Waziri na watendaji wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili la ardhi limekuwa na changamoto kubwa hususan katika kutatua migogoro kutokana na uchache wa watumishi kwenye Mabaraza ya Ardhi hususan Mabaraza ya Wilaya. Kwa mfano Wilaya yangu ya Ngara Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi Wilaya anahudumia zaidi ya Wilaya mbili, na hivyo kupelekea kesi kukaa muda mrefu bila kukamilika, na wananchi wanatoka maeneo mbalimbali na kutumia gharama kubwa hata kuweza kukata tamaa.
Ni lini Serikali itaweza uajiri Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi la Wilaya ya Ngara ili kuondoa usumbufu huu atakaekuwa yuko stationed katika Wilaya hiyo ya Ngara?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Gashaza ametaka kujua ni lini Wizara itapanga Mwenyekiti wa Baraza katika eneo lao, napenda tu nitoe taarifa kwamba upangaji wa Wenyeviti wa Mabaraza kutokana na uchache wa Wenyeviti tulionao unapangwa kutegemeana na wingi wa mashauri katika eneo lile. Lakini kwa habari tu nzuri kwenu ni kwamba sasa hivi tayari tumetangaza nafasi 20 tumepewa, kwa ajili ya kuajiri Wenyeviti watakaokwendakatika Mabaraza.
Kwa hiyo, kitakachofanyika ni tathimini kujua ni Wilaya ipi ina mashauri mengi na inahitaji kuongezewa nguvu na Wilaya zipi ambazo zinakwenda kuanzishwa ili kuweza kupewa Wenyeviti kama Wilaya ya Mbulu ambao huwenda wakapata Mwenyekiti kwa sababu ya shughuri hizo. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi tu kwamba tutalifanyia kazi na kuweza kujua kama watahitaji kuongezewa mtu mwingine.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi naomba nimuulize Naibu Waziri swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa mashamba mengi ya mkonge yalikuwa wanamilikiwa na wakulima wale wahifadhi wa mikonge. Lakini mashamba yale yamekuwa Mashamba pori na wananchi wengi na hasa wa hususa wananchi wa Korogwe wanahangaika mashamba ya kulima na mashamba yale hayaendelezwi. Je, Serikali ina mpango gani kurudisha mashamba haya kwa wananchi wa Korogwe ili nao wapate kulima?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake anataka kujua ni lini pengine yale mashamba ambayo yamekuwa mashamba pori hayaendelezwi tuweze kuyarejesha pengine kwa wananchi waweze kuyatumia.
Napenda tu nilifahamishe Bunge lako suala la kutambua shamba hili ni shamba pori, halijaendelezwa na limekiuka taratibu jukumu hilo analo Afisa Ardhi Mteule katika Halmashauri husika. Kwa hiyo ni jukumu la Halmashauri husika kuanza kufanya zile hatua za awali za kuweza kuchukua taratibu zote za kisheria, kuweza kuona kwamba huyu mtu amekiuka taratibu zake basi utaratibu wa kumnyang’anya unafuata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niwaombe sana kwa sababu tulishasema, ni jukumu la Halmashauri sisi kama Wizara mkishakamilisha kazi yetu ni kumshauri Mheshimiwa Rais kuweza kuyafuta na yanarudi kupangiwa matumizi. Lakini pia kwa nafasi hii nitoe rai mashamba yote yale ambayo yanafutwa na Mheshimiwa Rais, yakirudishwa katika maeneo yetu msiyapangie matumizi ya makazi mashamba yote kwa sababu sasa hivi unajikutakwamba hata pale ambapo panahitaji kuendeleza kilimo watu wanagawana mashamba. Kinachotakiwa eneo lile likisharudishwa lazima pawekewe mpango mzuri wa matumizi. Kama linaendelea kuwa shamba basi tuweze kujua ni mwekezaji yupi atafanya kazi hiyo, au kama mnabadilisha matumizi kwa sababu mengine yanakuwa yameshavamiwa na wananchi basi pia tuwe na utaratibu wa kuwa na akiba ya ardhi kwa baadae, lakini tuwe pia na kutenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji, ili tena tusije tukapata shida, Kwa sababu ardhi haiongezeki na watu wanaongezeka. Kwa hiyo ni jukumu la kila Halmashauri kuona namna bora ya kutumia Wizara tupo kwa ajili ya kutoa ushauri, kwa ajili kutoa Wataalam kuweza kufanikisha azma ya Halmashauri.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kati ya maeneo ambayo kulikuwa kuna viwanda vya Tanganyika Packers ni Jimbo la Kawe, Kata ya Kawe ambayo miaka sita iliyopita kwa kushirikiana na Serikali ya Awamu ya Nne tulifanikiwa kuliokoa eneo husika kutoka kwa waliokuwa wawekezaji uchwara na hatimaye Shirika la Nyumba la Taifa likakabidhiwa kupewa jukumu la kujenga Kawe Mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tokea Awamu ya Tano imeingia madarakani…
Mheshimiwa Mwenyekiti, tokea Awamu ya Tano imeingia madarakani, mradi ule ambao ulikuwa unahusisha nyumba zaidi ya 50,000 ni kama vile umekwama, matokeo yake eneo lile linakuwa kama sehemu ya genge la majambazi na wahalifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninataka Serikali iniambie, ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba ujenzi wa Kawe Mpya ya kisasa unafanyika kama ambavyo ilikuwa ni katika mpango wa miaka mitano na mwaka mmoja mmoja wa Serikali?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli mpango wa Serikali kujenga nyumba kama ilivyokuwa imepangwa kwa National Housing ulikuwa umepangwa na ulikuwa unaendelea vizuri, lakini mpango ule ulisimama baada ya kuja kuongeza nguvu katika ujenzi wa nyumba za Makao Makuu hapa Dodoma. Hata hivyo, kwa sababu suala zima la ujenzi wa nyumba za hapa Dodoma unaendelea vizuri, miradi mingine yote iliyokuwa imesimama sasa hivi wataanza kuitekeleza kwa sababu utaratibu tayari umeshawekwa vizuri.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, hata hivyo nina maswali mawili mafupi.
Swali la kwanza; katika baadhi ya Wilaya, Vijiji pamoja na Kata mpango huu wa kupima ardhi mpaka kupata hatimiliki unachukua muda mrefu kiasi wananchi wanasumbuka, wanahangaika wakifuatilia hati zao. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi hawa kusudi waweze kutumia muda mfupi wasitumie muda mrefu na Hatimiliki zao ziweze kupatikana kwa muda mfupi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; napongeza Serikali kwa kuanza kupima ardhi kwenye Mkoa wa Morogoro katika Wilaya za Ulanga, Kilombero pamoja na Mvomero; na huu mpango wa kupima ardhi unapunguza migogoro ya ardhi kwa upande wa wafugaji pamoja na wakulima.
Je, nauliza Serikali, mpango huu utakamilika lini kwa kupima ardhi kwenye Mkoa wote wa Morogoro kwenye Wilaya zake saba ambazo itasaidia kutatua migogoro ya ardhi ambayo imekithiri kwa muda mrefu katika Mkoa huu wa Morogoro? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA YA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza amesema kwamba mpango wa matumizi bora ya ardhi unachukua muda mrefu na hatimaye watu wanachelewa kupata hati zao. Napenda tu nilifahamishe Bunge lako, mpango wa matumizi bora ya ardhi hauwezi kwenda kwa kasi kama tunavyotarajia kwa sababu inategemea pia maridhiano kati ya wanakijiji na matumizi yao katika maeneo yale ambapo unapoandaa mpango huo lazima uhusishe makundi yote ya wafugaji, wavuvi na kila watu walioko pale na lazima pia waangalie ukubwa wa ardhi yao waliyonayo na mpango wanaotaka kuweka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima uende taratibu kuhakikisha kila mmoja ameshirikishwa na amekubaliana na mpango, sasa hatuwezi kwenda kwa kasi kwa sababu unashirikisha. Pengine labda elimu iendelee kutolewa hata kabla hatujafika sisi basi elimu iendelee kutolewa ili watu waone umuhimu wa kupanga mpango wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo yao ili kuepusha migogoro ambayo mara nyingi inajitokeza.
Swali la pili, Mheshimiwa Mbunge anaulizia ni lini tutakamilisha kupima ardhi yote katika Mkoa wa Morogoro na kuondoa migogoro iliyopo. Napenda nimhakikishie tu kwamba mpango wa Wizara tulionao siyo wa Morogoro tu, Morogoro ilikuwa ni eneo la mfano katika zile Wilaya tatu ambazo zilikuwa na migogoro pia ili kuweza kujua gharama za upimaji tukitaka kupanua mpango huu utatugharimu kiasi gani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naona kwamba zoezi lile pale limekwenda taratibu sana kwa sababu linahusisha Wananchi na pia kuweza kujua tunawezaje kukamilisha kupima katika nchi nzima. Ni mpango wa Wizara kuhakikisha kila kipande kinapimwa sasa uzoefu wa Morogoro utatusaidia ku-scale up upimaji na kuweza kujua gharama halisi zinazoweza kutumika na mpango huu tunaendelea nao na kwenye bajeti pia tumeonesha hivyo naomba tu Waheshimiwa Wabunge wawe na subira wakati Wizara inajipanga vizuri.
MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Takwimu ya ufaulu zinaonesha kuwa wanafunzi wa Serikali wanapata idadi ndogo ya ufaulu kuliko private. Hiyo inasababisha kupata nafasi ndogo ya udahili katika vyuo na inasababisha kupata watalaam wachache kutokana na uchache wa nafasi zao ya udahili.
Je, Serikali haioni kwamba inaweza ikapoteza watalaam kutokana na uchache wa wanaodahiliwa kwa kuwa wanafunzi wengi wa private wanaachwa kwa dhana kwamba wana uwezo wa kulipia ada za vyuo kutokana na uwezo wao uliokithiri wa kusoma katika shule hizo za private? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, miaka ya nyuma shule zilikuwa za sekondari na msingi zikifundisha masomo ya ufundi mbalimbali; uhonaji, useremala na kadhalika, je, Serikali ina mpango gani ya kuhakikisha inarudisha tena masomo haya ya ushonaji, ufundi mbalimbali kwa vitendo ili kuweza kuwawezesha wanafunzi wanapomaliza masomo yao wajiajiri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI (K.n.y. WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Nuru swali lake la kwanza amezungumzia habari ya takwimu ya wanafunzi wanaomaliza kwenye private school na wale wanaomaliza kwenye shule za Serikali. Naomba nimhakikishie kwamba hili suala ni la kitakwimu na anachokisema sidhani kama ana uhakika kwamba wa private ni wengi kuliko wale wa shule za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ni swali la kitakwimu, basi tutalichukua ili tuweze kuleta takwimu sahihi kulingana na alichokizungumza. Kwa imani natambua ya kwamba hakuna ambapo shule za Serikali zimekuwa nyuma sana ukilinganisha na za private kitakwimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili linazungumzia habari ya wanaomaliza ni namna gani wataweza kuendelezwa akirejea kwamba zamani mitaala ilikuwepo ya kufundisha useremala na mambo mengine. Naomba nimhakikishie kwamba Shule zetu au vyuo vyetu vya VETA zinafanya kazi hiyo ya kuweza kufundisha wanafunzi wanaoishia form four au darasa la saba mambo ya ufundi, lakini vile vile tuna vyuo 55 ambavyo vilikuwa ni Vyuo vya Maendeleo ya Jamii na sasa hivi kati yake karibu vyuo 20 vinakarabatiwa ili kuweza kufundisha ufundi stadi kwa wanafunzi wale ambao wanakuwa wameshindwa kuendelea na masomo ya sekondari aidha kwa A’ level au kwa form one.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Hivi sasa nchi nzima hatuna vitabu vya elimu ya msingi kwa darasa la nne hasa mitalaa mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wanafunzi hawa wanatarajia kufanya Mitihani ya Taifa hivi punde mwisho wa mwaka huu, Serikali ina utaratibu gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama majibu ya Serikali hayatatosheleza kwa umma wa Watanzania na sisi Wabunge, basi tuahirishe mjadala ulioko mezani tukajadili jambo hili kwa manufaa mapana ya nchi yetu. Naomba majibu ya Serikali.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI (K.n.y. WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA): Mheshimiwa Mwenyekiti, anachokizungumza Mheshimiwa Mbunge sidhani kama ni sahihi, kwa sababu ni karibu wiki mbili au tatu zimepita Wizara imesambaza vitabu vya darasa la kwanza mpaka darasa la nne kwa Halmashauri zote nchini. Sasa kwa hali hiyo, nina imani kwamba vitabu vipo katika mashule na hapana huo upungufu anaozungumza kwa sasa.
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri kwamba mtalaa wa shule binafsi na Serikali ni mmoja, lakini kwa zaidi ya miaka kumi shule za binafsi zimekuwa zikiongoza katika ufaulu.
Je, Serikali pamoja na kwamba inasema ina wajibu wa kusimamia kiwango cha ubora elimu nchini, haioni sasa ni wakati muafaka kujifunza kwa watu binafsi ni kwa namna gani wanafundisha watoto wao wanafaulu katika shule zao; badala ya kwamba Serikali inayosimamia ubora lakini shule zake zimekuwa zikifanya vibaya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI (K.n.y. WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, siyo kweli kwamba shule za binafsi zinafanya vizuri zaidi ya kuliko shule za Serikali. Ninachotaka kumhakikishia ni kwamba…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia idadi ya wanafunzi wanaokwenda kwenye shule za private ni wachache kuliko wanaokwenda kwenye shule za Serikali. Kwa hiyo, kwa vyovyote unapofanya rating ya wanafunzi, lazima pia uzingatie na wingi wa wanafunzi. Kwa hiyo, asilimia kumi ya wanafunzi 20 huwezi kulinganisha na asilimia kumi ya wanafunzi 1,000 kwa maana ya kwamba idadi inakuwa tofauti. (Makofi)
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mheshimiwa Sugu alivyosema mnasema hatupongezi lakini katika hili nimpongeze Waziri wa Ardhi pamoja na Naibu atleast wamefika maeneo mengi kufanya kazi yao vizuri. Kwa hiyo, kwa mazuri yanayofanyika sisi tunapongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu ni mawili. La kwanza, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba kwa sasa hakuna changamoto, nakubaliana kwa sehemu zimeondoka lakini malalamiko makubwa ya kampuni binafsi ni kwamba hawapati ushirikiano kwa watendaji wa Serikali kwa sababu wanaona kwamba wanachukua kazi zao. Kwa hiyo, wanapotoa taarifa kuomba vibali wale watendaji wakati mwingine wanawazunguka wanakwenda kuchukua kazi zao kwa sababu wanakuwa kama intruders kwenye kazi zao, Serikali itatatuaje tatizo hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili, Mheshimiwa Lukuvi mwaka juzi alizindua masterplan katika Manispaa ya Iringa na tulikuwa Manispaa ya kwanza kuzindua masterplan jambo ambalo ni jema, nimesema nalipongeza na tumeendelea kufanya kazi vizuri. Hata hivyo, hivi karibuni Mkuu wa Mkoa ametangaza katika Manispaa ya Iringa watu wajenge wanavyotaka hata kuingilia maeneo ya CBD. Je, Serikali inasemaje? Tumsikilize nani kati ya Waziri au Mkuu wa Mkoa? Bado niseme nawapongeza ningeomba nipate majibu ya Serikali kuhusiana na jambo kama hili.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza amezungumzia habari ya wapimaji binafsi ambao hawapati ushirikiano. Tatizo hilo hatujalipata kama Wizara na lengo la kuwaweka wao ni kuhakikisha kwamba upimaji unaongezeka. Sasa kama suala ni kuongeza kasi halafu wanapata vikwazo, tunahitaji tupate uthibitisho wa hayo ili tuweze kuyafanyia kazi lakini kwa sasa hatujapata malalamiko hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili la masterplan na Mheshimiwa RC kuingilia kazi hiyo, naomba kusema kwamba hilo pia nalo hatujalipata lakini masterplan ndiyo kiongozi wa kupanga miji kama ilivyo na Iringa kweli mmekuwa wa kwanza. Kwa hiyo, tunachosema masterplan ikishapitishwa inahitaji kutekelezwa kama ilivyo na siyo vinginevyo.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze Naibu Waziri pamoja na Waziri kwa jinsi ambavyo wanasimamia masuala mbalimbali ya Wizara hii vizuri, lakini pia nishukuru kwa haya majibu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya swali hili bado changamoto zipo, bado kuna watu wanaokiuka huu mwongozo wa Wizara. Sasa ningependa kujua, Wizara iko tayari kufanya utafiti ili kujua ni maeneo gani katika nchi hii, Mikoa gani, Wilaya zipi ambazo bado taasisi za Serikali, watu binafsi wanakiuka mwongozo huu wa Wizara na kuchukua hatua stahiki ili kuondoa hii kero kwa Wananchi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ziko taasisi, ziko Halmashauri ambazo pia hazifuati utaratibu wa namna ya kuchukua maeneo ya wananchi. Kwa mfano katika jimbo langu, Kata ya Kirongo, Samanga, Kijiji cha Kiwanda, eneo la Mteri, Mkurugenzi alikwenda kuchukua ardhi ya wananchi ili kupata eneo la kujenga Ofisi ya Wilaya, lakini amewaacha wananchi katika malalmiko makubwa sana kwa sababu, hakuwahusisha kijiji, kata wala Halmashauri.

Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri, uko tayari ukipata nafasi uje Rombo ili twende pale tusaidie kutatua hili tatizo ili kuondoa hayo malalamiko kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameongelea habari ya taasisi ambazo zinakiuka utaratibu, kwanza nipokee shukrani ya pongezi zake kwa niaba ya Waziri kwa Wizara, lakini pia nijibu swali lake ambalo ameongelea taasisi ambazo zinakiuka utaratibu kwa kukiuka.

Kwa hiyo, mimi niseme tu kwamba pale ambapo inatokea taasisi yoyote au watu binafsi wanapotwaa maeneo kwa kukiuka utaratibu au mwongozo tulioweka tunaomba tupate taarifa mapema ili tuweze kuichukulia hatua kwa sababu si rahisi kuweza kujua kwamba wapi na wapi wamekiuka kama hatukuletewa taarifa. Kwa hiyo, mimi naomba hilo liweze kufikishwa ili tuweze kulifanyia kazi. Nitoe rai tu kwa taasisi zote kuzingatia taratibu na miongozo iliyowekwa katika utwaaji wa maeneo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili amesema baadhi ya Halmashauri kutozingatia utaratibu wa kutwaa maeneo na akatolea mfano eneo la Kironga Somanga kule kwake.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa Halmashauri zote na tumeishatoa utaratibu, ni marufuku kutwaa ardhi ya mwananchi yoyote kwa sasa kama hakuna fidia ya kulipa. Kwa hiyo ni lazima kwanza fidia ipatikane ndipo uweze kutwaa ardhi, kwa sababu tumekuwa na changamoto nyingi kuna watu wengi wanadai fidia kutokana tu na taratibu zilikiukwa katika kuchukua maeneo. Kwa hiyo sasa hivi tumesema hatutaki kuongeza migogoro, unapotaka kutwaa ardhi ya eneo lolote lazima taratibu zizingatiwe na lazima kuwa na mazungumzo na wahusika wenye ardhi.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nitakuwa mchoyo wa fadhila kama nisiposhukuru kwa kweli kwa utayari wa Serikali kuanzisha Baraza la Ardhi la Wilaya ya Mbulu.

Mheshimiwa Spika, lakini bado, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri ameonesha katika majibu yake ya msingi kwamba kuna changamoto hizi za watumishi na kwa kuwa wananchi wa Mbulu bado watakuwa wanakwenda Babati ambaki ni mbali kwa kutafuta hiyo huduma. Je, ni lini sasa ataanzisha Baraza hili ili wananchi hao wasisafiri umbali mrefu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa wataalam walishakuja kuangalia maeneo ya kuanzisha Baraza hilo na tumeshawapa na jengo na kwa kuwa Wilaya ya Mbulu ni kubwa. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari sasa kuja kuangalia na kuona eneo gani sahihi la kuanzisha barabara hilo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameuliza ni lini Baraza hili litaanzishwa. Katika majibu yangu ya msingi nimesema tayari Serikali imeshatupa Wizara Wenyeviti 20 ambao watapunguza kero katika baadhi ya Mabaraza ambayo hayakuwa na Wenyeviti wa kutosha, lakini pia kuna wale ambao hawakuwa na Wenyeviti kabisa watapelekwa. Kwa hiyo, mimi nimesema kwamba tayari Wenyeviti wapo, wanachosubiri kufanya sasa ni kupata tu maelekezo ya awali (induction course) kidogo ili waweze kwenda kufanya kazi zao, wakati wowote Baraza litaanza.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ameuliza kwamba Baraza hilo litawekwa wapi. Naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakwenda katika eneo husika kwanza kujiridhisha na jengo lililoandaliwa, lakini pia na eneo lililopo. Kwa hiyo nitafika Mbulu ili kuweza kuona eneo sahihi ni lipi ambalo tutaweka baraza na wananchi hawatapata usumbufu.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Spika, migogoro ya wakulima na wafugaji katika Mkoa wa Morogoro umetokana hasa na kutokuwepo na mipango mizuri ya matumizi ya ardhi. Maeneo yanayofaa kwa kilimo wamepewa wafugaji na maeneo yanayofaa kwa wafugaji wamepewa wakulima. Je, Serikali inampango gani kuainisha upya maeneo hayo ili kuwapa wananchi na kuondoa hii migogoro?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa migogoro hii ya wakulima na wafugaji mingi imechangiwa na Watendaji wa Ardhi katika Vijiji na Kata: Serikali haioni sasa kuna haja ya kuwalipa fidia wananchi ambao wamebaki na makovu kutokana na migogo hii?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameongelea habari ya matumizi bora ya ardhi katika maeneo na amesema kwamba maeneo ya ufugaji wamepewa wakulima na maeneo ya wakulima wamepewa wafugaji.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda nimdhibitishie Mheshimiwa Mbunge kwamba upangaji wa matumizi ya ardhi haufanywi na Wizara. Upangaji wa matumizi wa ardhi, mdau wa kwanza ni mwananchi wa eneo husika. Tunapokuja ku-facilitate lile zoezi la upangaji, wananchi wenyewe wanakuwa wameshaainisha maeneo yao kwa ajili ya ufugaji na maeneo kwa ajili kilimo. Kwa hiyo, kinachofanyika pale ni kuweka mipaka kwa maana ya kwamba maeneo ya ufugaji yafahamike na maeneo ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pale inapotokea vurugu, ni kati ya watumiaji wa ardhi wanapokiuka makubaliano ya awali, kwamba mfugaji anatoka kwenye eneo lake la ufugaji anakwenda kwenye maeneo ya kilimo; au mtu wa kilimo anakwenda kulima kwenye maeneo ya wafugaji. Kwa hiyo, mgogoro mkubwa ulioko hapa ni kwa watumiaji wa ardhi.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai tu katika maeneo yote yenye migogoro kati ya wakulima na wafugaji na ambapo mpango wa matumizi bora ardhi umepangwa, waheshimu maamuzi ambayo wameyafikia wao wenyewe na yanakuwa yameingia katika mpango wa matumizi bora ya ardhi. Kwa hiyo, hili ni jambo la watumiaji ardhi ambapo tunasisitiza waheshimu pale ambapo haijafanyika. Kwa wale ambao hawajapanga matumizi bora ya ardhi, basi nitoe rai tu kwamba mpango huo ufanyike na Wizara ipo tayari kwa ajili ya kuratibisha zoezi hilo ili angalau wananchi wote waweze kuwa na maeneo yao yaliyopangiwa matumizi kuepuka hii migogoro na inapotokea wanakiuka utaratibu, basi sheria ziweze kuchukuliwa.

Mheshimiwa Spika, swali lingine amesema Watendaji ambao wanachangia pengine kupata migogoro na licha ya hivyo kunakuwa na fidia za watu, niseme kwamba Watendaji hao kama wapo, ndiyo maana Wizara kuna baadhi ya Watendaji imewasimamisha kazi na wengine wameondolewa kwa kukiuka maadili ya utendaji wao.

Mheshimiwa Spika, suala la kusema kwamba kunakuwa na suala la kulipa fidia, hilo ziwezi kulitolea maamuzi sasa kwa sababu hatujawa na changamoto nalo kama Wizara na kuangalia hasa changamoto hii imetokana na nini? Kwa Watendaji waliokiuka taratibu zao, hatua zinachukuliwa. Sasa hivi tunamshukuru Mungu kwamba angalau wameanza kuwa na maadili kiutendaji tofauti na siku za nyuma.
MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Ukiangalia bajeti ambayo imekuwa ikitengwa kila mara kwa ajili ya hii kazi ya kupima matumizi ya ardhi ni ndogo sana. Mpaka sasa miaka 57 ya uhuru tumepima asilimia 15 tu ya nchi ya Tanzania na migogoro bado ni mingi kila siku kukicha kuna migogoro. Je, Waziri atakubaliana nami kwamba, kwa style hii migogoro haitaisha na kwamba, nchi itakuwa haina amani na utulivu kwa sababu ya migogoro ya ardhi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni mikoa mingapi ambayo mpaka sasa hivi imeanzisha Benki za Ardhi ili kurahisisha uwekezaji na pia kuwawezesha wakulima wakubwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Nyongeza ya Mheshimiwa Ruth Mollel kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza anasema bajeti ni ndogo kiasi kwamba, migogoro bado inaongezeka kuwa mingi na huenda pengine ikasababisha kutokuwa na amani. Katika jibu langu la msingi nimeonesha takwimu ikionesha bajeti ilianza kiasi gani na sasa iko kiasi gani. Ilianza na bilioni 1.5 lakini sasa hivi tumefikia bilioni 6. 3. Kwa hiyo, ni vitu ambavyo vinaongezeka mara kwa mara, lakini kama hiyo haitoshi Wizara yangu inalo jukumu la kuwezesha halmashauri katika kuwapa uwezo wa kuweza kusimamia masuala ya mpango wa matumizi bora ya ardhi ili kuhakikisha kwamba, eneo lote linapimwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hii imekuwa ikifanyika na mpaka sasa tunapoongea jumla ya vijiji 1,880 vimekwishafanyiwa mpango wa matumizi bora ya ardhi na sasa hivi tunazo wilaya kama 40 ambazo mpango bado unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo ni kwamba, pale ambapo halmashauri zinawezeshwa tuna imani kwamba, zoezi la upimaji litaendelea na sio kusubiri Wizara kwa sababu, sheria yenyewe inatamka wazi kwamba, mamlaka za kupanga na kupima maeneo ni halmashauri zetu za wilaya na vijiji katika maeneo. Kwa hiyo, ni jukumu pia la halmashauri zetu na sisi pia tukiwa ni washiriki katika mabaraza yetu, basi tusimamie zoezi hilo ili kila halmashauri iweze kutekeleza wajibu wake ambao inapaswa kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kuhusu kuainisha ni mikoa mingapi, naomba swali hili nisimjibu kwa sababu linahusu takwimu, pia niweze kuwa na uhakika ni kiasi gani, nisije nikampa jibu lisilo sahihi. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nataka nimfahamishe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inatambua umuhimu wa kupanga na kupima kila kipande cha ardhi. Ndio maana mwaka huu tumeamua kuandaa mradi mkubwa ambao utatuwezesha katika miaka mitano hii tuwe tumekamilisha upimaji na upangaji, upangaji na upimaji kila kipande cha ardhi nchini. Kwa hiyo, pamoja na hiyo fedha ya bajeti ya Serikali ya kawaida tumeamua tukope kwa sababu, ina faida kubwa zaidi kwa kupanga na kupima nchi nzima kwa wakati mmoja kwa sababu, vilevile tunajua itatusaidia katika kupata mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mwananchi akimiliki kwa hati, atalipa kodi kila mwaka, kwa maana hiyo kila mtu atafaidika na upangaji na upimaji. Kwa hiyo, pamoja na hiyo ya bajeti, lakini Serikali tumeamua kuanzisha huo mradi mkubwa wa kupanga na kupima kila kipande cha ardhi na mradi huo utaanza mwaka huu baada ya Bajeti ya Serikali ya mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeanza majaribio wilaya tatu, Kamati yetu ilikwenda juzi kuangalia namna tunavyoweza kufanya. Wameridhika na taarifa imetolewa jana kwamba, jambo lile linawezekana tukiwa na uwezo wa kutosha. Kwa hiyo, kutokana na ule mfano tulioufanya katika Wilaya tatu za Mkoa wa Morogoro tunataka kuusambaza nchi nzima mijini na vijijini. Kwa hiyo, jambo hilo Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge tunalifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tumefanya uwezeshaji mikoani kwa kununua vifaa, jambo moja linalowafanya Halmashauri washindwe kupima na kupanga ni vifaa. Serikali, kupitia Wizara yangu, tumeshanunua vifaa vya kutosha vya upimaji ambavyo kila halmashauri inayotaka kupanga na kupima maeneo waende kwenye kanda wakaazime bila kukodisha ili viwasaidie katika zoezi la upangaji na upimaji kwenye wilaya zao.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsnate sana. Tangu alipouziwa hilo shamba, leo ni miaka 12, lakini mpaka leo hajaendeleza hata ekari moja, imekuwa ni shamba pori na kusababisha vijiji vilivyozunguka hilo shamba vya Sikaungu, Songambele na Msanda Muungano kukosa sehemu ya kulima. Mkoa wa Rukwa, wananchi wote wanategemea kilimo, sasa kwa nini wanasitasita wasimpelekee Mtukufu Rais kulifyekelea mbali hili shamba, kulifuta kama alivyofuta mashamba mengine?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Hilo shamba linamilikiwa na Halmashauri ya Sumbawanga DC na Manispaa. Cha ajabu, vigezo gani vilitumika, mkataba uliingia peke yake na Manispaa ya Sumbawanga kuuza hilo shamba bila Manispaa ya Sumbawanga DC kushirikishwa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Ally Keissy kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ufutaji mashamba halianzii kwenye Wizara ya Ardhi, suala la ufutaji mashamba kama halijaendelezwa wahusika wa kwanza ni zile mamlaka zenyewe za upangaji miji katika maeneo yao. Kwa hiyo, kama wao waliona kwamba hili shamba pengine halijakidhi vigezo, linatakiwa kufutwa, walitakiwa wao walete mapendekezo hayo kwa Waziri na Waziri angemshauri Mheshimiwa Rais kulifuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hiyo haitoshi, walikuwa pia na mgogoro naye na walipelekana Mahakamani. Halmashauri yenyewe husika ikatoa shauri Mahakamani na wakakubali ku-settle nje ya court. Kwa hiyo, sisi kama Wizara hatuwezi kuingilia makubaliano yao. Kwa hiyo, kama bado wanaona hajaendeleza, basi warudi tena wao wachukue maamuzi kama waliyokuwa wamechukua mwanzoni ya kuchukua hatua. Wakileta, sisi tutashughulikia vinginevyo itakuwa kidogo ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili anaongelea kwamba shamba lile linaingia katika Halmashauri mbili; nadhani katika ziara yangu niliyofanya mwaka 2017 suala hili nililipata na nililitolea maelekezo. Nilisema kama pale ambapo unakuta shamba la mwekezaji limeingia katika Halmashauri mbili tofauti, ni jukumu la Halmashauri husika kuzungumza naye kuweza kuona ni namna gani Halmashauri zote mbili zitafaidika na mwekezaji huyo kama ameingia katika maeneo yao. Sasa sisi kama Wizara hatuwezi kuwapangia namna ya kukubaliana, kwa sababu ni mazungumzo kati ya mwenye eneo na mwenye mamlaka ya upangaji miji na yule mwekezaji aliyeko katika eneo lao. Kama itashindikana, wanahitaji ushauri kutoka Wizarani, tuko tayari kuwasaiia kwa suala hili.
MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami niulize swali dogo la nyongeza. Kumekuwa na migogoro ya muda mrefu sana katika Jimbo la Mikumi, hasa kwenye Kata ya Kilangali kati ya wananchi na SumaGrow; Kata ya Masanze kati ya Miyombo Estate na wananchi; Kata ya Tindiga kati ya Mauzwi Estate na NARCO na wananchi lakini pia Kata ya Kisanga Estate na wananchi pamoja na WEDO na Stignati:-

Je, Serikali imejipanga vipi kumaliza migogoro hii ambayo ipo katika Jimbo la Mikumi ambayo kwa kweli inahatarisha sana maisha ya wananchi wa Jimbo la Mikumi?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro hii ameileta hapa na hatujajua wao wenyewe wamefikia wapi. Kwa sababu migogoro mingi Wizara inaingilia kati pale ambapo Halmashauri inakuwa imeshindwa. Mheshimiwa Mbunge amezungumza ni migogoro ya muda mrefu lakini katika ile migogoro ambayo tuko nayo mgogoro anaotaja hatuko nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwahidi tu kwamba kama kuna migogoro kati ya wawekezaji na kata alizozitaja, basi tuko tayari kusaidiana nao kuitatua ili mradi tu tuweze kujua wao wenyewe wamefikia wapi. Kwa sababu mazungumzo lazima yaanzie kwenye eneo husika. Wizara haiwezi kuingia moja kwa moja mpaka ijue wapi wamekwama. Hatujalipokea na wakilileta tutalifanyia kazi.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali dogo la nyongeza. Matatizo yaliyoko huko kwenye Shamba la Efatha Mkoa wa Rukwa yanafanana kabisa na matatizo yaliyoko katika Halmashauri ya Itigi shamba lililokuwa linamilikiwa na shirika ambalo limekufa la Tanganyika Packers. Serikali haitoi tamko la moja kwa moja, liko chini ya Msajili wa Hazina, lakini hakuna mwekezaji aliyejitokeza hadi leo hii.

Je, Serikali imekubali sasa kulirudisha shamba hili kwa wananchi kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Itigi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli suala analolizungumzia Mheshimiwa Massare ni la muda mrefu, lakini naomba tu nimpe uhakika kwamba masuala yote ambayo yanasimamiwa na Msajili wa Hazina alishaanza kuyapitia na kuweza kuona mashamba yale au uwekezaji ambao ulikuwepo na ukakwama uko chini ya Hazina sasa hivi, anapitia shamba moja baada ya lingine na akishakamilisha basi anaweza kutoa nini kitawezakufanyika. Hatuwezi kusema sasa hivi kwamba tunalirudisha kwa wananchi wakati Msajili wa Hazina bado anafanyia kazi mashamba hayo.
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Waziri ambayo kimsingi hayajaonesha kutatua migogoro ya ardhi katika Taifa hili, swali la kwanza; migogoro hii imekuwa ni mingi katika mikoa, hususan Mikoa ya Dar es Salaam, Katavi, Mwanza na maeneo mengine. Cha kushangaza, majibu haya ya Serikali yanasema kwamba wametenga shilingi bilioni nne. Lengo hapa ni kutatua, kwamba wanapokuwa wanawaondoa wananchi kwenye maeneo yao, kwa sababu Serikali ndiyo inakuwa imefanya uzembe kuwashirikisha wananchi moja kwa moja kuwaondoa katika maeneo yao lakini pia katika suala la kuwalipa fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kata ambazo zimeathirika katika Manispaa ya Mpanda ni Kata ya Misunkumilo ambayo iliondolewa na Jeshi, Kata ya Shanwe ambayo ilipisha ujenzi wa barabara lakini pia Kata ya Uwanja wa Ndege ambayo kulikuwa na ujenzi wa Chuo cha Kilimo. Sasa wananchi hawa wanapata shida na hawaelewi hatma yao ya kulipwa fidia zao. Sasa Serikali imepanga nini ii kulipa wananchi hao?

swali la pili ni suala la upimaji shirikishi. Serikali imekuwa ikitoa vifaa kama alivyosema Mheshimiwa Waziri, lakini hakuna ushirikishwaji wa moja kwa moja kwa wananchi kwa maana ya kwamba wanapima maeneo yao lakini kwa wananchi ambao wanakuwa hawana pesa ya kulipia viwanja, angalau basi Serikali ione namna ya kuweza kuchukua; kwa mfano, kama mwananchi ana viwanja vitatu au vine, basi anapimiwa eneo lake na anapewa hatimiliki ili baadaye aweze kulipa hiyo fedha au achukuliwe baadhi ya viwanja ili kukamilisha mchakato wa ulipaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nimfahamishe Mheshimiwa Rhoda kwamba Serikali imeshachukua hatua za dhati kuhakikisha ya kwamba migogoro yote ya ardhi iliyoko kati ya wananchi na Taasisi mbalimbali ikiwemo Jeshi na wengineo inafikia ukomo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameunda Tume ambayo ina Mawaziri wanane, ambao wamepitia maeneo karibu ya mikoa yote na kuweza kupitia maeneo yenye migogoro ili waweze kumshauri Mheshimiwa Rais nini kifanyike katika maeneo hasa ambayo yamekuwa na migogoro mingi. Kwa hiyo, kama kuna eneo lake ambalo pia lina mgogoro na Wanajeshi, nadhani hilo linachukuliwa hatua na baada ya muda siyo mrefu, basi Serikali itatoa maelekezo nini kifanyike katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile katika suala la kusema kwamba unamwachia mwananchi eneo lake, nadhani Halmashauri nyingi; nimepita katika mikoa zaidi ya 18 na nikatoa maelekezo na nilikuta wengine wameshaanza kufanya kazi yao vizuri. Mfano mzuri ni Halmashauri ya Kalambo ambao walikuta kwamba tayari wana makubaliano na wananchi, wanamwachia asilimia 60 na wao wanachukua 40; na ile asilimia wanammilikisha yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lililopo kwa wananchi wetu, hata ungempa yote, hawezi kuilipia yote. Tumewaelekeza ya kwamba lazima ifanyike kama walivyokubaliana na ukishaipima ile ardhi inakuwa imeshaongezewa thamani. Kwa hiyo, hata kama atauza, yeye mwenyewe hawezi kumiliki, tayari umeshaongeza thamani na iko katika mpango ambao ni wa kimipango miji, kwa hiyo, haiwezi tena kuwa na ujenzi holela.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba tu Halmashauri zisimamie mambo haya kwa sababu ziko Halmashauri nyingi ambazo zinafanya wakiwemo Chemba na wengineo ambako tumepita.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nasisitiza Mheshimiwa Mbunge afuatilie kwenye Halmashairi yake ambayo ni Mamlaka ya Upangaji. Alichosema kwamba Serikali imetoa shilingi milioni nne, siyo shilingi milioni nne, ni shilingi 6,400,000,000/= ambazo zimekwenda kwenye hizo Halmashauri nilizotaja. Tuna imani wakizitumia vizuri wakapanga miji yao, suala la ujenzi holela halitakuwepo.
MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwa kuwa Serikali imekiri kwamba kuna hiyo haja ya kupima upya hayo mashamba yaliyotaifishwa na kwamba jukumu hilo lipo kwenye Halmashauri, lakini kama inavyofahamika, sasa hivi Halmashauri nyingi nchini zina hali mbaya sana ya kiuchumi ikiwa ni pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Moshi Vijijini.

Je, Serikali iko tayari kutoa fedha kwa namna ya upendeleo, kama tutatenga fedha kwenye Halmashauri kwa ajili ya kuharakisha huo upimaji? Kwa sababu tatizo kule ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Katika hayo mashamba yaliyotaifishwa, yapo mashamba ambayo yamegawanywa kabisa kwa ujumla na matumizi yakabadilika, kwa hiyo, wamiliki ni wapya kabisa. Sasa kila wakijaribu kuomba kupimiwa upya inakuwa ni tatizo kwa sababu zile hati za awali hazijafutwa. Mfano hai ni shamba moja kule Uru lililokuwa chini ya Chama cha Msingi Uru Kati, shamba linaloitwa Kosata. Mfano Shule ya Sekondari ya Uru Seminari imeshaomba kwa zaidi ya miaka kumi kupimiwa lakini hati ile haijafutwa.

Je, Serikali itafuta lini hizo hati za mashamba ya aina hiyo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anauliza kama Wizara ni lini itaweza kusaidia Halmashauri ambazo pengine zipo duni kiuchumi kwa ajili ya kuweza kuongeza kasi ya upimaji. Naomba niseme, jana wakati najibu swali moja hapa nadhani la Mheshimiwa Joyce, nilitoa kwa ufafanuzi mkubwa sana kwamba pamoja na kwamba mamlaka za upangaji miji ni Halmashauri zenyewe, lakini wizara imeweka juhudi kubwa kuhakikisha kwamba inazipa support kubwa ya kuwawezesha kuweza kupima maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juhudi kubwa ya kwanza ambayo tulifanya ni kuweka vifaa vya upimaji katika kanda zote na vifaa vile vinatolewa bure katika Halmashauri na inasaidia katika kupima kwenye Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tulitoa pesa, shilingi bilioni 6.4 na nimesema jana, katika Halmashauri 25 ambazo tunawasaidia kwa ajili ya upimaji, wamechukua zile pesa ili kuweza kuongeza kasi ya upimaji. Kwa hiyo, Halmashauri yake kama nayo ni mhitaji, nadhani tutaangalia uwezekano kwa kipindi kinachokuja tuweze kuona ni jinsi gani tutawawezesha ili waweze kupima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe Halmashauri zote wanatakiwa kutenga bajeti kwenye bajeti zao kwa ajili ya kuongeza kasi ya upimaji kwenye maeneo yao ili kupunguza migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ameongelea suala la shamba lile la ushirika ambalo kuna maeneo yamegawiwa kwa taasisi nyingine kwa mfano Jimbo Katoliki la Moshi wamepewa eneo hilo, Uru Seminari ambayo ameisema wamepewa eneo hilo lakini hawajaweza kumilikishwa kwa sababu nyaraka zinasemekana kwenye kile Chama cha Ushirika zimepotea. Mwezi Februari mwaka 2019 wametoa taarifa rasmi Polisi kuonyesha kwamba zimepotea. Sasa huwezi kumilikisha mtu mwingine wakati ile hati nyingine iliyokuwepo bado haijafutwa na haijaweza kupatikana kiasi cha kuweza kuwapa hati wale wengine. Kwa hiyo, kinachofanyika sasa baada ya ule utaratibu wa kisheria kukamilika, basi na hawa wengine ambao wamepewa maeneo yale katika lile shamba lililokuwa awali lililobadilishiwa matumizi, nao watapata. Pia kwa sehemu kubwa inaweza ikafanyika kwenye zoezi la urasimishaji kwa sababu tayari kuna maeneo mengi yameshajengwa hospitali, shule na makazi. Kwa hiyo, hilo litafanyika kulingana na taratibu za kisheria mara taarifa zilizopelekwa Polisi zitakapokuwa zimefikia hatima yake. Ahsante.
MHE. SONIA J. MAGOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Wilaya ya Handeni ni Wilaya kubwa sana lakini kwa bahati mbaya hawana Baraza la Ardhi kiasi kwamba yanapotokea matatizo yanayohusu ardhi inawabidi wananchi kusafiri mpaka Wilaya ya Korogwe:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia wananchi hawa Baraza la Ardhi?

Swali la pili; kumekuwa na migogoro ya muda mrefu katika Vijiji vya Sezakofi Kata ya Ndolo, Wilaya ya Handeni na Kata ya Kwagunda Wilaya ya Korogwe:-

Je, Mheshimiwa Waziri ni lini atakwenda kuwaona wananchi hawa ili kusikiliza kero zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza Mheshimiwa Sonia ameuliza ni lini tutaweka Baraza la Ardhi katika Wilaya ya Handeni, kwa sababu sasa hivi wanakwenda Korogwe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tu nimfahamishe kwamba ni dhamira njema ya Serikali kuhakikisha kwamba inakuwa na Mabaraza ya Ardhi katika kila Wilaya. Mpaka sasa tuliyonayo kisheria ni mabaraza 97 ambapo 53 yanafanya kazi na 44 hajaweza kuanza kufanya kazi. Tatizo kubwa lililopo katika uanzishwaji wa mabaraza, jambo la kwanza ni ile rasilimali watu wa kuweza kuhudumia mabaraza hayo lakini pia na maeneo au majengo kwa ajili ya kufanyia shughuli hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, pia tunapeleka baraza pale ambapo pengine pana mashauri mengi kiasi kwamba panahitaji nguvu ya ziada. Ni hivi karibuni tu tumeongeza mabaraza mengine likiwemo la Mbulu na maeneo mengine kwa sababu tu tayari tulishapata nafasi ya ofisi katika eneo lile na sisi jukumu letu kama Wizara ni kupeleka watumishi pamoja na samani za ofisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutaangalia tawimu zilizopo kwa Handeni kama kweli ni nyingi kiasi cha kutaka kuwa na baraza, basi nitawaomba uongozi wa pale watuandalie eneo ambalo litakuwa ni ofisi linalokidhi vigezo vya kuwa Baraza la Wilaya. Vinginevyo nitawaomba waendelee kutumia Baraza la Korogwe kwa sababu lipo karibu na bado hawana mashauri mengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ameuliza ni lini nitakwenda katika eneo la Handeni kwenye Kata ya Sasako na Kwagunda kwa ajili ya kutatua migogoro. Naomba nimthibitishie tu kwamba ni dhamira njema ya Wizara kuhakikisha kwamba tunafika maeneo yote yenye migogoro lakini kabla hatujafika, uongozi uliopo katika maeneo yale unafanya kazi nzuri sana ya kuweza kutatua migogoro. Pale ambapo inashindikana na uongozi uliopo pale, basi Wizara ipo tayari kufika. Kwa kesi yake huyu, basi tutaangalia uwezekano wa kuweza kwenda kutatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Mbunge wa eneo lile, Mheshimiwa Mboni, amekuwa akiulizia pamoja na jirani yake Mheshimiwa Kigoda, nikawaambia tutafika pale. Nilikuwepo mwaka 2016 lakini nitatafuta muda tena kama bado kuna kero, tutaenda kuzitatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, nataka kutoa nyongeza nimfahamishe Mheshimiwa Sonia kwamba takwimu zinaonyesha kwamba mashauri mengi ya ardhi yalikuwa yanatoka Wilaya ya Lushoto ndani ya Mkoa wa Tanga. Kwa hiyo, Serikali hivi sasa imefanya jitihada ya kuongeza Baraza jipya la Lushoto ili kupunguza load ya mashauri ndani ya Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivi sasa tumeanzisha baraza, ukiacha Korogwe ambao walikuwa wanahudumia mpaka Lushoto, sasa Lushoto wanajitegemea. Kwa hiyo, kwa kufanya hivyo maana yake hata Handeni sasa mtapata huduma nafuu zaidi kwa sababu nusu ya matatizo ya kero ya ardhi ya Tanga sasa yamepatiwa ufumbuzi kwa kumpeleka Mwenyekiti mpya Wilaya ya Lushoto.
MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Naomba nitumie fursa hii kwanza kuipongeza sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua kubwa ambayo Wizara imekuwa ikiendelea kufanya hasa katika zoezi zima la kutoa notice kwa wakulima wakubwa wenye kuhodhi maeneo makubwa. Nami ni shahidi kabisa kwa Jimbo la Handeni Vijijini, zoezi hili limekuwa linaendelea kwa kasi na limepelekea wananchi wa Jimbo la Handeni sasa kujikita sana kwenye kilimo cha muhogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe tu ushuhuda hasa kwenye Kata ya Kabuku na Mkata sasa hivi zoezi hilo linaendelea na Halmashauri imekuwa ikipambana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nitumie fursa hii kumwomba Mheshimiwa Waziri, kasi hii iweze kuendelea kwa sababu Handeni, hususan Jimbo la Handeni Vijijini tuna maeneo makubwa sana japokuwa mpaka sasa kwa kusema kweli nitoe tu ushuhuda kwamba hakuna conflict ya maeneo. Wananchi wameendelea kujitoa sana na kilimo cha muhogo na mpaka sasa hivi ni mashahidi kwamba Handeni tunaongoza kwenye kilimo cha muhogo na tunapata viwanda ambacho Serikali kupitia Balozi wetu wa nchini China wametuletea kiwanda cha mihogo ambacho tunategemea hivi karibuni kitaanza kujengwa.

MWENYEKITI: Haya ahsante.

MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu; naomba sana Mheshimiwa Waziri aweze kutuambia zoezi hili litaendelea mpaka lini kwa sababu wananchi wa Jimbo la Handeni wanaendelea kuwa na chachu kubwa sana ya kuweza kupata. Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mboni Mhita, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze na nimshukuru kwa kupongeza Serikali, lakini niseme tu kwamba zoezi hilo aliloliuliza nadhani sio kwa Handeni peke yake, zoezi hili linatakiwa kufanyika nchi nzima. Zoezi hili linatakiwa kufanywa na halmashauri husika zenyewe, wao ndio wenye maeneo, ndio wanajua nani kaendeleza, nani hajaendeleza. Kwa hiyo nitoe rai kwa halmashauri zote; jukumu lenu ni kuhakikisha mnafanya ukaguzi wa mara kwa mara kwenye mashamba ya wawekezaji ambao hawajaweza kuyaendeleza. Wakituletea taarifa Mheshimiwa Waziri atamshauri Mheshimiwa Rais kuyafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunapokea kutoka kwao, Wizara sio inayoanzisha ufutwaji wa mashamba au ukaguzi unafanywa na halmashauri husika. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, jukumu hili ni la halmashauri, naomba walitekeleze na sisi kama Wizara tuko tayari kuwasaidia kumshauri Mheshimiwa Rais.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nina swali dogo la nyongeza; tatizo la Baraza la Ardhi kwa Mkoa wa Kigoma ni tatizo sugu na mashauri mengi ya ardhi katika Mkoa wa Kigoma yapo katika Wilaya ya Kasulu, wameshafanya utafiti wa kuanzisha baraza pale lakini huu ni mwaka na nusu sasa. Je, ni lini wanatuanzishia Baraza la Ardhi Kasulu ili kupunguza matatizo ya ardhi na watu wasiende Kigoma na wengine kutoka Kibondo kwenda Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika mabaraza mapya ambayo yameanzishwa nadhani na Kasulu limo kama kumbukumbu zangu ziko vizuri. Kwa hiyo nasema tutafika tuweze kuona eneo ambalo limeandaliwa kwa ajili ya baraza kwa sababu katika yale yaliyoongezeka nadhani na Kasulu imo. Ahsante.
MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana Serikali kwa majibu mazuri na yenye kutoa matumaini lakini pamoja na hayo nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ni dhahiri kuwa mashine hii ingetumika vizuri ingesaidia sana kuondoa upungufu mkubwa sana wa majengo mbalimbali yanayohitajika katika kila sekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kuwa Serikali imekubali kuwa sasa iko tayari kushirikiana na Wizara nyingine kuhakikisha kuwa mashine hii inatumika vizuri zaidi. Je, ni lini sasa huo mkakati utafanywa kwa ajili ya kuhakikisha kuwa upungufu wote wa nyumba za watumishi, madarasa, zahanati unafanyiwa kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kiasi kikubwa teknolojia hii ni mpya na haijulikani vizuri, wako tayari kuitangaza ili hata private sector waitumie?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Janet Mbene, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipokee shukurani alizozitoa kwa kazi ambayo inafanyika kwa kuona kwamba kuna umuhimu wa kutumia mashine hizo. Kama nilivyojibu kwenye swali la msingi y kwamba upungufu unaokuwepo pale ni fedha za maendeleo, kama zingepatikana kazi hii ingeweza kuendelea vyema na nyumba nyingi zingejengwa kwa kutumia mfumo huo lakini kwa sababu pesa ni kidogo unakuta haiendi sambamba na mahitaji yaliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ni kwamba Serikali iko tayari kwa maana ya Wizara kushirikiana na Wizara zingine kuweza kufanya kazi hiyo. Kama Wizara zingine zitakuwa zipo tayari pengine kugharamia material yale ambayo yana bei kubwa basi Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa liko tayari kushiriki katika ujenzi kwa sababu ndio wenye teknolojia hiyo.
MHE. YOSEPHER F. KOMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikiliza Waziri wakati anajibu, nafahamu Wilaya ya Muheza ni moja kati ya wilaya ambayo iliyofutiwa hati mashamba zaidi ya sita toka wawekezaji ambao mengi yao yalikuwa mashamba ya mikonge. Kutokana na hilo kumekuwa na tatizo kubwa sana la migogoro, sasa naomba niulize kuhusu kwanza watumishi, Serikali imejiandaaje hasa kwa mwaka huu inatuambia nini wananchi wa Muheza kwenye suala la watumishi, tutawaongezea watumishi wangapi ukizingatia tatizo la watumishi linatuathiri sana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Rais alipokuwa anaenda kuzindua bomba la mafuta kule Tanga alipopita Muheza aliahidi na aliwaambia wananchi watagawiwa maeneo bure walime na kuyaendeleza, lakini wananchi wa Muheza hawakuamini hivyo, wamekuwa wanalipishwa gharama za upimaji na wamekubali. Hata hivyo, kuna migogoro mikubwa sanasana, wafanyakazi wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza wanaohusika na ardhi wamekuwa wanauza maeneo ya wananchi kwa watu tofauti ambao siyo wakazi wa Muheza. Nataka nipate kauli ya Serikali, je, wapo tayari kutuma timu maalum iende Muheza ikasimamie masuala ya ugawaji wamashamba na viwanja hasa katika maeneo haya sita ambayo yamefutiwa hati?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri katika swali lake la msingi, lakini naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yosepher kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la watumishi nadhani hata kipindi kilichopita Bunge lililopita tulilizungumzia kwamba baada ya watumishi sasa kuelekezwa kwenye Wizara ya Ardhi, tayari tulikuwa tunafanya utaratibu wa kupata ikama yao na kujua wanataaluma tulionao ni kiasi gani ili waweze kusambazwa katika Halmashauri kulingana na uhitaji na kazi hiyo inafanywa na Ofisi ya Rais, TAMISEMIkwa sababu suala la uhamisho litasimamiwa na Wizara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika suala zima la ugawaji wa mashamba na wakati tumeenda kwenye ziara ya Kamati ya Ardhi suala hilo tulilikuta, lakini tayari Ofisi ya Halmashauri pale Muheza walikuwa wameshaanza kugawa hekari tatu tatu kwa wananchi katika yale mashamba yaliyorejeshwa na suala la kulipishwa katika suala la upimaji ni makubaliano ya Halmashauri yenyewe ambayo walikaa wakakubaliana na kiasi cha wao kuchangia na ndicho hicho kilichofanyika. Kwa hiyo suala linalofanyika linafanyika kutegemeana na mamlaka zenyewe za upangaji na matumizi bora ya ardhi. Kwahiyo hilo ni suala ambalo lipo chini ya halmashauri na Serikali inalisimamia kulingana na makubaliano ambayo yanakuwa yamefikiwa, hakuna migogoro ambayo itaendelea kwa sababu kila kitu kinasimamiwa.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Migogoro ya ardhi katika nchi hii ipo katika kila wilaya na kila mkoa, lakini katika Mkoa wetu wa Songwe mpaka sasa hivi hatujapata Baraza la Ardhi la Wilaya na Wilaya zetu za Ileje Momba na maeneo mengine zinakwenda Mbeya Mjini. Je,ni lini Serikali sasa itaanzisha Baraza la Ardhi la Wilaya katika Mkoa wetu wa Songwe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Meshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakajoka kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ambayo Serikali inatakiwa kufanya kazi kila wilaya inapaswa kuwa na Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya na tayari tulishasema na kutoa majibu tuna mabaraza 97 ambayo tayari yalikwishaanzishwa na sasa hivi yote yatakwenda kufanya kazi kwa maana ya kwamba tumepata baadhi ya watumishi ambao wanakwenda. Hata hivyo, kufungua Baraza la Ardhi katika eneo inategemeana pia na idadi ya kesi na namna ambavyo wilaya yenyewe imejiandaa katika kutupa ofisi, kwa sababu katika maeneo ambayo tunafanyia kazi hiyo, Wizara haijengi ofisi bali Halmashauri na mkoa husika wanatupa majengo, sisi tunapeleka watumishi pamoja na vitendea kazi, kwa maana ya thamani. Kwahiyo kama watakuwa tayari, basi tunaweza tukafika katika eneo hilo, lakini pia tunazingatia takwimu na migogoro iliyopo. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi. Naipongeza Serikali kwa upande wa Morogoro kwa kuanza upimaji wa ardhi hasa kwa upande wa Wilaya za Malinyi, Kilombero na Ulanga, lakini upimaji unakuta migogoro bado inaendelea kwenye Wilaya nyingine, lakini ni matatizo kweli kwa vifaa vya upimaji kwa sababu vinanunuliwa kwa bei ghali na halmashauri zingine hazina uwezo wa kununua hivyo vifaa. Je, Serikali inasemaje kwa kusaidia hizo Halmashauri ambazo haziwezi kununua hivyo vifaa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ishengoma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipokee shukrani zake kwa Serikali kwa kazi inayofanya katika Wilaya ya Malinyi, Ulanga na Kilombelo, kwa kupima ardhi yote katika maeneo yale na niwashukuru wananchi wa maeneo hayo kwa sababu wamekuwa wakitoa ushirikiano mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kumaliza migogoro hiyo kama ambavyo tumeanza ile ni kama pilot area, lakini tayari tutakuwa na resource persons wengi kutokana na wananchi wenyewe kwa sababu pia watakuwa wamepata ujuzi mzuri wa kuweza kufanya scale up kwenye maeneo mengine na lengo la Wizara ni kuhakikisha maeneo yote yanapimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vifaa vya upimaji, napenda nitoe rai kwa halmashauri zetu zote, Wizara ilikwishatoa vifaa katika maeneo yote ya kanda zetu nane, lakini halmashauri haziendi kuomba vifaa vile. Bahati nzuri kwa kuwa ameuliza hili swali, basi nitatayarisha takwimu niletehapa baada ya kuwa tumeshapata vifaa, ni halmashauri ngapi zimeomba. Halmashauri nyingi hawaendi kuchukua vifaa, lakini wana-opt kutafuta vifaa vya kukodi wakati kuna vifaa vya bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwa halmashauri zetu, watumie vifaa hivyo ambavyo Wizara ilishafundisha watumishi wawili, wawili kutoka kila halmashauri kwa nchi nzima ambao wana Wapima kwa ajili ya kuweza kutumia vile vifaa. Matokeo yake wamefundishwa, hawaleti maombi na vifaa vimekaa idle,halafu Wabunge wanalalamikia suala la upimaji. Naomba usimamizi katika halmashauri, watumie vifaa ambavyo tayari Wizara imegharamia.Ahsante.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sanakwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Lupembe katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe haina Afisa Ardhi Mteule na tuna mpango wa kupima ardhi katika maeneo yetu.

Je, ni lini Serikali italeta mtaalam kwa maana ya Afisa Ardhi Mteule ili kuweza kusaidia kupima ardhi lakini pia kutatua migogoro iliyopo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hongoli kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani wakati najibu swali nyongeza la Mheshimiwa Yosepher, nimesema utaratibu unafanyika sasa tutaweza kuwatawanya wataalam wetu kama walivyo, lakini kwa sasa naomba tu waendelee kumtumia huyo Afisa Ardhi Mteule ambaye alikuwa kazi yote kutoka kwenye halmashauri jirani ya jimbo lake ili tuweze kuendelea. Hii kazi itakamilika muda si mrefu, naomba tu Waheshimiwa Wabunge tuvumiliane kwa sababu kazi ya kuwapanga itachukua muda kwa sababu yakutaka kujua taaluma zao na uhitaji wa kila halmashauri.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niulize maswali ya nyongeza mawili kama ifutavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimhakikishie Naibu Waziri aliyejibu maswali pamoja na Bunge kwa ujumla kwamba Mgogoro bado upo kati ya magereza na Kijiji cha Tumaini. Na uthibitisho ninao naomba nikukabidhi vithibitisho nilivyonavyo. Wananchi wanajua haki zao wanajua beacons zilizowekwa na baadaye kuondolewa, kwa hiyo mgogoro bado upo sasa maswali mawili kama ifuatavyo:-

(i) Kwa kuwa Serikali inasema imemamliza mgogoro wananchi wa kijiji cha Tumaini wanasema mgogoro bado upo. Je huoni kwamba kuna umuhimu wa wewe mwenyewe kwenda kuangalia nani anayesema ukweli na kutatua tatizo hili?

(ii) Kwa kuwa urambo kuna migogoro mingi kuhusiana na mipaka na hata ile inayopakana pori la akiba la ugala ikiwemo sehemu Indenda, Lunyeta, Uyumbu, Tevela pamoja na Ukondamoyo.

Je huoni Mheshimiwa Waziri kwamba utakapokwenda kutatua tatizo la Tumaini na magereza pia utatue migogoro mingine iliyopo hapa na ninapendekeza pia kwamba ufuatane na Waziri wa Maliasili kwa sababu pia vinahusiana pamoja?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kulikuwa mgogoro kama ambavyo nimeeleza katika jibu langu la msingi na mgogoro huo ulitatuliwa lakini tukumbuke tu kwamba vijiji hivi vilipimwa mwaka 2013. Lakini wakati huo gereza lile lilipimwa mwaka 1988 maana yake gereza lilitanguliwa likiwa na ekari 10,416 baada ya kuwa na mgogoro walipunguza kiasi cha ekari 7,198 kama nilivyotaja kwa vijiji ambavyo nimevitaja kwenye jibu la msingi la gereza likabaki na ekari 3,218.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa akilifuatilia hili suala la mgogoro na ana vielelezo vingi vya wananchi wake wakilalamika nipende kumkubalia alichosema kwamba twende pengine tukaangalie uhakika uliopo nasema nipo tayari kwenda kwa ajili kuangalia mgogoro uliopo ili tuweze kuumaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili alikuwa anaongelea mgogoro wa mipaka katika maeneo mengine ambao yanaingiza kwenye pori la akiba sasa niseme hili pia katika ule msafara wa mawazie nane walikuwa wakipitia migogoro hii yote ilikuwa imehusisha Wizara ya Maliasili, TAMISEMI lakini wakati huo huo aridhi na Mambo ya Ndani pia walikuwapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, cha msingi hapa ni kufanya ufuatiliaji wa kina kwanza tuone hivi vijiji alivyovitaja vya Senda, Tundu na Ukomola kama vipo kwenye vile vijiji 366 ambavyo vilikuwa vimeainishwa katika kile kitabu kibwa cha migogoro. Kama napo kutakuwa kuna shida basi nitakapokuwa nina-solve mgogoro wa hili gereza na vijiji vya tumaini basi tutafika na hili pori la akiba tuweze kuona nini cha kufanya. Ahsante.
MHE. SABREENA H. SUNGURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Wazaramu wana msemo wao unaosema kwamba: “Zilongwa mbali, zitendwa mbali”. Ukiangalia majibu haya na uhalisia kwa wananchi ni vitu viwili tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa suala zima la watu kupatiwa Hatimiliki Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana alitangaza kwamba wananchi waache kutumia offer na waingie kwenye mfumo huo rasmi wa kutumia Hatimiliki na wananchi walifanya maombi kwa muda mrefu sana. Katika Kanda mbalimbali kumekuwa kuna unreasonable delay ya kutolewa kwa vitu hivi ambavyo wanajua ni vya msingi na vinawafaa sana wananchi wetu na vinatakiwa vitolewe kwa wakati. Je, Wizara sasa iko tayari kuunda tume kuchunguza maafisa wa Serikali ambao wanaharibu mpango huu mzuri wa Serikali kwa makusudi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tunaelewa kabisa kwamba sasa hivi kama nchi inajipanga irudi kuendesha bajeti zake kwa kutumia vyanzo vyetu vya ndani na Serikali imekuwa ikipata mapato kupitia urasimishaji wa Hatimiliki na vilevile hata pale inapofanya transfer au sale, imekuwa ikipata mapato kama capital gain tax ambayo ni 10%, stamp duty, registration fee na kadhalika. Je, kwa kuchelewesha kuwapa huduma hizi kwa wakati muafaka kutokana na majibu haya ndani ya siku saba mpaka mwezi mmoja hawaoni kwamba wanaisababishia Serikali hasara hasa ikizingatiwa umuhimu wa Wizara hii ambapo kikatiba majukumu haya amepewa Mheshimiwa Rais na yeye ameyagawa kwa Makamishna wa Wizara ili waweze kumsaidia?

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sabreena, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza ameongelea habari ya ucheleweshaji, pengine watumishi hawafanyi kazi zao vizuri kiasi cha kuchelewesha Hati kutoka na hivyo kuwanyima haki wananchi. Naomba nimthibitishie tu kwamba katika zoezi zima la utoaji Hati toka tumebadili muundo ndani ya Wizara katika kufuatilia kwa karibu mpaka sasa baadhi ya Kanda zina Hati zaidi ya maelfu ambazo hazijachukuliwa, kwa mfano, Dar es Salaam (7,000), Tabora (12,000) na Mwanza (7,000). Kwa hiyo, kasi ya utoaji Hati ni kubwa lakini pia wananchi hawazichukui.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe rai tu kwamba wazifuate Hati zao ili waweze kuwa na umiliki ulio na salama zaidi. Watumishi sasa hivi wamebadilika siyo kama ilivyokuwa zamani. Nikiri mwanzo kidogo kulikuwa na ucheleweshaji lakini baada ya kuwa na mkataba kwa mteja kazi inaenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la siku saba au thelathini ni kwamba hatutaki kumsumbua mwananchi. Kwa mfano, katika ile njia ya elektroniki ambayo inatumika Dar es Salaam Hati inaweza ikatoka ndani ya siku mbili au siku moja lakini hatutaki kumcheleweshea kwa sababu kunakuwa pengine na mlolongo wa watu ambao wako pale kuliko asubiri pengine amekuja asubuhi itatoka saa nane, basi tunampa siku ili apate muda wa kuja kuchukua. Kwa kutumia njia ya elektroniki Hati inaweza ikatoka kwa siku moja kama taratibu zote zimezingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili anaongelea habari ya mapato, ni kweli mapato yanaongezeka kadri ambavyo utoaji hati unafanyika. Hata hivyo, napenda kumthibitishia tu kwamba katika usajili wa Hati mbalimbali ambazo zinafanyika, Wizara imekuwa ikifanya usajili katika nyaraka mbalimbali. Ukiangalia kuanzia Julai, 2018 mpaka Juni, 2019, Hati za kumiliki ardhi zilizotolewa ni 49,892 kwa kipindi cha mwaka mmoja. Pia ukiangalia milki zilizofanyiwa transfer nazo ni 2,998. Vilevile kuna hizo nyaraka ambazo ameziongelea pale wanapokuwa wana-surrender nazo tumeshasajili 2,632.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna mlolongo mrefu ambao tumefanya ambapo unaingizia mapato Serikali. Sasa hivi wananchi wamekuwa makini katika kufuata taratibu, hawafanyi tofauti na kile ambacho wanaelekezwa na wengi wanakuja ofisini. Kwa hiyo, niseme mapato yameongezeka na wananchi sasa wanatumia ofisi zetu vizuri tofauti na walivyokuwa wakifanya awali.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na swali la msingi linalohusu Baraza la Kata, pia Mkoa wetu wa Songwe hauna Baraza la Ardhi la Wilaya. Nimekuwa nalalamika sana kwenye Bunge hili na Mheshimiwa Naibu Waziri alijibu kwamba jambo hili watalishughulikia haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi wananchi wangu wa Songwe wanakwenda Mbeya kusikiliza kesi zao na inasababisha gharama kubwa sana za kwenda kufika kule kusikiliza kesi na kurudi.

Je, ni lini Baraza la Kata litaanzishwa katika Mkoa wetu wa Songwe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa mujibu wa Sheria, tunatakiwa kuwa Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya kila Wilaya. Mpaka sasa Mabaraza yaliyoanzishwa kisheria yameshafikia 100, lakini yanayofanya kazi yako 54.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema kwamba tuko tayari kuanzisha Baraza katika Wilaya yoyote ili mradi pawepo na miundombinu ambayo itawezesha kuanzishwa kwa Baraza hilo. Kwa sababu kama Wizara, hatujengi majengo kwa ajili ya Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya. Kwa hiyo, kama wakiwa tayari; na nilipokuwa kule mwezi uliopita, waliitoa hoja hiyo, nikasema tunachohitaji ni kuonyeshwa eneo ambalo litatosheleza kuweza kuwa na Ofisi ya Baraza la Ardhi na Nyumba ya Wilaya. (Makofi)
MHE. MARY D. MURO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa muda wa kuuliza swali la nyongeza. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa shirika lilishajenga nyumba tayari na zimekosa wanunuaji, je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba zile nyumba zinanunuliwa, itapunguza bei au itafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kujenga nyumba nyingi vile bila kuangalia mahitaji ya soko, je, Serikali haioni kama inapoteza hela za wavuja jasho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Muro kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimthibitishie kwamba hakuna nyumba zilizokosa soko mpaka muda huu. Nyumba zote ambazo zilijengwa kwa ajili ya kuuzwa baada ya kuona watu hawawezi kununua kwa kiasi kile ambacho tulitarajia, nyumba zote zile zimepangishwa na kama zipo ambazo hazijapangishwa ni chini ya asilimia mbili. Hiyo imetokana tu na namna ambavyo mahitaji yalivyokuwa yakiombwa awali kwa sababu maeneo mengi ambapo nyumba zilijengwa awali yalikuwa ni mahitaji ya halmashauri husika, waliomba kujengewa, lakini baadaye hawakuchukua. Kwa hiyo shirika limeamua kuzipangisha nyumba zile na sasa hivi zote zimepangishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lake la pili anazungumzia habari ya mahitaji ya soko. Mahitaji ya soko ya nyumba bado ni makubwa sana. Kwanza tukiangalia tunahitaji kuwa na nyumba walau milioni tatu ambazo tunatakiwa tujenge walau nyumba 200,000 kila mwaka, hatujaweza kufikia idadi hiyo. Kwa hiyo, bado mahitaji ni makubwa zaidi kuliko ambavyo tunatarajia na ndiyo maana sasa kuna nyumba za gharama nafuu zitaendelea kujengwa katika maeneo mbalimbali tukianza na hapa Makao Makuu ya nchi.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika swali la msingi iliulizwa kuhusu Shirika la Nyumba la Taifa na ujenzi wa nyumba za gharama nafuu. Katika Jimbo la Kibamba, Shirika la Nyumba la Taifa lilikabidhiwa eneo kubwa kidogo kwa ajili ya ujenzi wa Mji wa Viungani wa Luguruni kwa maana ya Luguruni Satellite Town ambayo ingehusisha nyumba za gharama nafuu, nyumba za kupangishwa, nyumba za kibiashara na miundombinu mingine. Hata hivyo, kwa miaka mingi pamoja na National Housing kupewa jukumu la kuwa mwendelezaji mkuu mpaka sasa hakuna chochote kilichoendelea na kimsingi eneo lile limeanza kugeuka kuwa kijipori.

Je, ni lini hasa National Housing itatekeleza huu wajibu wa kwenda kuujenga Mji wa Luguruni ikiwemo ujenzi wa nyumba za gharama nafuu?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnyika kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli National Housing wana eneo kule Luguruni na walikuwa wamepanga kujenga Satellite City kama ambavyo mkakati ulivyokuwa umepangwa. Eneo hilo halijajengwa mpaka sasa si kwamba limetelekezwa, isipokuwa katika ujenzi, bado kuna utaratibu ambao unaendelea katika kuhakikisha kwamba miradi yote ambayo ilikuwa inasimamiwa na imepangwa kujengwa, inajengwa. Kwa hiyo eneo lile mpaka sasa taratibu ziko vile vile na tungependa kutoa rai watu wasivamie eneo kwa sababu bado matumizi yapo pale pale kama ilivyopangwa. Nami nimhakikishie tu baada ya hii miradi mingine inayoendelea kukamilika, mji ule utajengwa kama ilivyokuwa imepangwa.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongeze kidogo kwamba maeneo mengi ambayo yamechukuliwa na National Housing nchi hii, mengine tumeweka kama Land Bank ya Serikali kwa sababu National Housing ndiyo mwendelezaji mkuu wa miliki kuliko waendelezaji wengine. Sisi tulijua lile eneo tusingelichukua sisi leo lisingekuwepo na ndiyo maana kwa sababu tumelichukua sisi hakuchukua mtu binafsi, tumeweza kuwapa hawa Ubungo eneo la kujenga wilaya pale Luguruni hivi sasa. Tumeweza kuwapa watu wa MSD kujenga ghala kubwa, walikuwa wanatumia zaidi ya bilioni tatu kupanga kwa ajili ya kuweka dawa lakini tumeweza kuwapa pale. Kwa hiyo wasichukulie tu kwamba maeneo tunayachukua National Housing ni kwa ajili ya uendelezaji wa haraka, lakini tuliya-protect kutokana na manyang’au wanaotaka kulangua ardhi zote za msingi katika maeneo ya miji na kuweka Land Bank.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana kwa taarifa yake Mheshimiwa nataka nimhakikishie kama isingekuwa National Housing kuchukua lile eneo wao wasingepata mahali pa kujenga Makao Makuu ya Wilaya.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri ni kweli kwamba kwa Jiji la Dar es Salaam tunajua kwamba population ni kubwa sana lakini National Housing wamechukua maeneo na hasa eneo la Kawe ambalo ni Satellite City na walishaanza ujenzi pamoja na pale Morocco Square. Nataka kujua, ni kwa nini ujenzi huo umesimama na ni lini wataendeleza ili wananchi wa Dar es Salaam waweze kupata makazi salama? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Susan Lyimo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli miradi ile ilianza na ikawa imesimama na ilisimama tu sio pengine kwamba National Housing wameshindwa kuendeleza, lakini kulikuwa na taratibu za kisheria ambazo zilikuwa zinafuatwa ili kuweza kukamilisha. Napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kuanzia sasa ataona miradi ile inaendelea tukianza na Morocco Square kwa kutumia mapato ya ndani ya National Housing wanakwenda kujenga majengo yale na kukamilisha, kwa hiyo hatutakuwa na viporo tena. Tunamaliza Morocco Square then tunaenda kule seven eleven ya Kawe. Hayo yote yako kwenye Mpango na Bodi mpya ambayo inafanya kazi hiyo imeweka Mpango Kazi wa kuhakikisha miradi viporo yote ya National Housing inakamilika kutokana na schedule walivyojipangia. Kwa hiyo niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge, miradi hiyo yote inakwenda kuanza kukamilishwa.
MHE. STANSLAUS S. MABULA:Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nitumie nafasi hii pia kumshukuru sana Naibu Waziri pamoja na Waziri kupitia Wizara ya Ardhi kwa kazi kubwa ambayo kwa kweli katika suala zima la urasimishaji makazi wamejitahidi.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu kubwa ilikuwa ni namna gani wakazi hawa walioko kwenye maeneo ya milima watapatiwa nafuu kubwa hasa angalau kwa kutambulika. Sasa niishukuru Serikali kwasababu imeliona hili na kulifanyiakazi; ni jambo jema sana na mimi nawashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali inaendelea na utaratibu wa urasimishaji wa makazi, na tunafahamu kwamba ili urasimishe makazi yako maeneo ambayo yalikuwa na michoro ambayo ilikuwa na maeneo mbalimbali. Kwa mfano, maeneo kwa ajili ya maziko, kwa maana ya Makaburi; Serikali ina mpango gani sasa? Maana kumekuwa na mgogoro mkubwa, kwamba eneo lilitengwa kwa ajili ya makaburi lakini linakuta wananchi wameshajenga sana kwasababu halikulindwa na badala yake wanalazimika aidha sasa tuamue wananchi waondoke tubakishe eneo kwa ajili ya makuburi au wananchi wabaki ili tutafute eneo lingine la makaburi. Maeneo ya kule Sawa, Mwalukila pamoja na Igwambiti liko tatizo la namna hii; na namshukuru Waziri amefanya jitihada kubwa amefika kule.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili; ili uweze kupima na kupanga unahitaji fedha na Serikali imekuwa na utaratibu wa kutoa fedha kwenye halmashauri zetu kama mkopo. Sisi kama Wilaya ya Nyamagana, Jiji la Mwanza tulishaomba fedha na mikataba yote ikafungwa kwa ajili ya kupata fedha bahati mbaya sana hatujapata fedha hizi mpaka leo ni nini kauli ya Mheshimiwa Waziri? Ni lini tutapata fedha hizi hizi ili tupime na kupanga maeneo ambayo tunadhani yanaweza kuiingizia Serikali na Halmashauri mapato?(Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ili uweze kupima na kupanga unahitaji fedha na Serikali imekuwa na utaratibu wa kutoa fedha kwenye Halmashauri zetu kama mkopo.

Sisi kama Wilaya ya Nyamagana, Jiji la Mwanza tulishaomba fedha na mikataba yote ikafungwa kwa ajili ya kupata fedha bahati mbaya sana hatujapata fedha hizi mpaka leo. Ni nini kauli ya Mheshimiwa Waziri kwamba lini tutapata fedha hizi ili tupime na kupanga maeneo ambayo tunadhani yanaweza kuiingizia Serikali na Halmashauri mapato? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Stanslaus Mabula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Mabula kwa namna ambavyo amekuwa akipigania watu wake kwa ajili ya kurasimishiwa maeneo. Wote kama mnavyojua, Mji wa Mwanza umezungukwa na milima usipokuwa makini unaweza ukapata ajali kwa ajili ya watu pengine kuporomekewa mawe na kadhalika lakini amekuwa mvumilivu, amefuatilia na kuhakikisha kwamba taratibu zilizopangwa na Serikali zinafuatwa, namshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali yake mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza anazungumzia habari ya maeneo ya maziko ambayo tayari yameshavamiwa na ni kweli nilitembelea katika eneo lile nikakuta sehemu kubwa ya eneo lililokuwa limetengwa kwa ajili ya maziko limevamiwa na watu. Nitoe rai kwa Halmashauri zote kusimamia maeneo haya kwa sababu tunapanga maeneo hatuyasimamii matokeo yake watu wanavamia halafu kuwatoa inakuwa ni kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, lakini katika eneo alilolisema kwenye Kata ya Sawa, kuna maeneo ambayo yako wazi kidogo ambayo hayajavamiwa na kama wako watu hawazidi watano, bado tunaweza tukafanya mabadiliko katika ramani ya eneo lile ili watu wakapangwa kwenye maeneo yale wakaendelea na maisha yao halafu sehemu ya maziko nayo ikapatikana kwa sababu huduma zote tunazihitaji. Kwa hiyo, hilo ni suala la kumuelekeza Mkurugenzi wa Mipango Miji aweze kusimamia shughuli hiyo ili upangaji ufanyike upya katika eneo lile tupate eneo la maziko na watu warasimishiwe maeneo yale waweze kuishi kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anazungumzia suala la Halmashauri kuwezeshwa ili waweze kupata pesa za upimaji. Napenda tu nitoe taarifa kwenye Bunge lako, Wizara ilitoa zaidi ya shilingi bilioni 6.2 katika Halmashauri zipatazo 24 kwa ajili ya kuwapa mkopo usio na riba ili waweze kupima na kurejesha na wengine waweze kupewa. Nasikitika kusema kati ya Halmashauri 24, ni Halmashauri tatu tu ambazo zimeanza kurejesha mikopo yake. Kati ya hizo shilingi bilioni 6.2 ni shilingi milioni 906 ndiyo zimerejeshwa ambapo Halmashauri ya Ilemela imerejesha shilingi milioni 800 kati ya shilingi bilioni 1.5 iliyopewa; Halmashauri ya Ukerewe imerejesha shilingi milioni 20 kati ya shilingi milioni 73 na Halmashauri nyingine ambazo zimepelekewa bado hazijarejesha mpaka leo.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai ili na wengine waweze kufaidika na pesa hiyo tunaomba sana Halmashauri hizi waweze kurejesha pesa hizo ili wale wengine waweze kupata. Sifa ni moja tu, ni kuandika andiko ambapo utaonesha mchanganuo mzuri namna utakavyofanya upimaji wako, utakavyolipa fidia na utakavyorejesha mkopo. Kwa hiyo, ni kitu kidogo tu watu wanafahamu wafanye kazi hiyo na Wizara itapokea lakini kwa kusubiri pesa zirejeshwe.
MHE. ENG. RAMO M. MAKANI: Mheshimimiwa Spika, nakushukuru, napongeza pia kwa majibu mazuri ya Serikali, hata hivyo nina maswali ya nyongeza mawili, swali la kwanza kuhusiana na kipengele (a) cha swali langu ili wataalam waweze kufanya kazi zao vizuri na watoe matokeo yanayostaili wanapaswa kutosha kwa idadi, pia wanapaswa kutosha kwa umahili wao yaani vile competence ya utaalam aliyonayo, pia wawe na maadili ya kitaaluma. Bila shaka ni ukweli kwamba wakiwa wachache hawawezi kukamilisha matakwa hayo.

Je, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru inaupungufu wa wataalam wa Sekta ya Ardhi, kwa zaidi ya asilimia 81 na kwa kuwa Serikali ina mpango wa muda mrefu wa kuendelea kutumia bajeti ya kila mwaka. Je katika mpango wa muda mfupi ambao ni wa kuwapanga upya watumishi katika nchi nzima Serikali iko tayari kuweka upendeleo maalum kwa halmashauri ya Wilaya ya Tunduru kwa sababu ya changamoto zilizopo hivi sasa?

Mheshimimiwa Spika, swali la pili katika kipengele (b) cha swali langu naona hapa kuna haja ya kupambanua iko shida ya kupata ukweli na uhakika, familia ya watu wanne inayotanjwa inamiki sehemu ndogo sana ya hili eneo ni kama eka 40 tu kati ya zile eka 1,913, eneo kubwa zima linalalamikiwa na halmashauri ya Kijiji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hata kesi inayotajwa siyo kesi ambayo inahusika mahali hapa sasa mimi nafikiri wakati tunaendelea kusubiri kupata uhakika juu ya umiliki wa eneo hili na hapa nitatoa ushauri kwa ufupi. Kwa nini tusiendane na maagizo ya Serikali maagizo ya Chama cha Mapinduzi kupitia ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo kwa kujibu wa Ibara ya 37 inasema Serikali inatakiwa kutekeleza maagizo ya Chama cha Mapinduzi kupitia ilani yake kwamba ni lazima kufanya uhakiki wa mashambapori yasiyoendelezwa kwa kipindi kirefu na kuyagawa upya kwa wananchi. Sasa eneo hili la eka 2,000 kwa zaidi ya miaka 20 limebaki tu likiwa halifanyiwi kazi…

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Injinia sasa swali.

MHE. ENG. RAMO M. MAKANI: Mheshimimiwa Spika, je Serikali iko tayari sasa kuunda timu maalum kwenda kufuatilia jambo hili kwa nini linachukua miaka mingi bila kupatiwa ufumbuzi huku eneo hili likiwa likitumika kienyeji na baadhi ya watu ikiwa ni pamoja na kuwafanya wananchi walime kwenye eneo hilo katika sehemu ndogo na kuwatoza mazao yanayolimwa katika eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimimiwa Spika, kwanza nikiri wazi kwamba kuna upungufu mkubwa kwa nchi nzima kwa watumishi wa Sekta ya Ardhi. Ukiangalia takwimu za mahitaji tuliyonayo tunatakiwa kuwa na watumishi 2,957 kwa nchi nzima; lakini mpaka sasa tunao 1,546 na hivyo tuna upungufu wa 1,411. Kwa hali hiyo upungufu uko maeneo mengi na kwa Mheshimiwa Engineer Ramo anao watumishi wanne ni kweli ni wachache, lakini kuna halmashauri inawatumishi wawili na nyingine tuliwahi kukuta ina mmoja. Nimuombe tu awe mvumilifu na Waheshimiwa Wabunge wote kwa sababu zoezi hili tumesema tunalipitia upya kwa kuangalia wale tulionao kwa sasa tunaanza kuwapanga upya ili kuweza kuleta uwiano wa kiutendaji katika halmashauri zetu.

Mheshimimiwa Spika, kwa hiyo, nimuombe sana pamoja na kuomba upendeleo nadhani tutaangalia wakati tunapanga tuweze kuona hasa maeneo ya pembezoni ambapo mara nyingi watumishi wengi wanakwepa kwenda kule. Kwa hiyo, tutaangalia na kuwapa umuhimu wale ambao tunajua wanayo shida kubwa katika Sekta hii ya Ardhi.

Mheshimimiwa Spika, jambo la pili swali lake la pili amezungumzia kwamba ile kesi pengine ni ya watu wanne na ni tofauti na suala la wanakijiji. Kesi ile imewekwa kwenye jibu la msingi kwa sababu ndiyo hasa ilikuwa imekwambisha katika mambo yote kufanyika pale, na wale walipofungua kesi maana yake hata Kijiji kisingeweza kufanya jambo lolote kwa sababu eneo lililokuwa linagombewa ni hilo la Kijiji.

Mheshimiwa Spika, lakini tumeshaona hitaji la eneo lile kwamba wananchi wanalalamika na bahati nzuri nakumbuka kama siyo mwaka jana nadhani mwaka juzi nilikwenda pale nikafika mpaka kwenye Kijiji nikafikia kile kilio cha wananchi. Kama Serikali tuliahidi kwamba tutalifanyia kazi na baada ya kukuta kuna kesi na maamuzi yalikuwepo tukawa tumefungwa mikono hatukuweza kufanya ile. Lakini kwa sababu pia kuna agizo la Serikali la kupitia mashamba pori yote na kuweza kuyaletea maelekezo yake kwa maana ya kuleta maepndekezo kwa Mheshimiwa Waziri ili yaweze kufutwa jukumu la kufanya hivyo ni la Halmashauri yenyewe ya Tunduru, ikisha fanya hivyo pamoja na halmashauri zingine chanzo lazima kianzie kwenye halmashauri husika ndipo wizara itaendeleo.

Mheshimimiwa Spika, kwa hiyo, nitoe rai kwa mara nyingine tena kwamba suala hili linahitaji kuanzia katika halmashauri zetu mkileta kwa Waziri, Waziri atamshauri Mheshimiwa Rais kuyafuta pale ambapo tunakuwa tumejiridhisha. Na nitoe rai ni marufuku kwa Serikali yoyote ya Kijiji au kwa watu wote wachache kutumia ardhi ya Umma katika kuwafanya watu kuwa kama vibarua kwa sababu unapompa mtu ardhi na kumtoza pesa maana yake wewe tayari umeshakuwa bepari wa kutaka kunyonya wengine. Ni marufuku na kama kuna maeneo watu wanatozwa pesa kwa matumizi ya ardhi kwa maeneo ambayo wameshindwa kuyaendeleza wenyewe tupate taarifa ili tuweze kuyafanyia kazi.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, pamoja na majibu hayo ya Serikali ninayo maswali mawili ya nyongeza. Changamoto kubwa ya upatikanaji wa hatimiliki za ardhi ni pamoja na gharama kubwa zinazohusu upimaji wa maeneo. Jambo ambalo wananchi wengi wanalishindwa hasa pale ambapo upimaji unatakiwa ufanyike kwa kundi kadhaa kubwa la wananchi ili yapimwe kwa pamoja. Kwa nini Serikali isipunguze gharama hizo ili wananchi waweze kupata fursa ya kumiliki ardhi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Waziri wa Ardhi Mheshimiwa Lukuvi alipokuwa Karatu tarehe 07 Machi, mwaka huu aliagiza kufutwa kwa hatimiliki ya ekari 20 katika Kitongoji cha Ngorongoro, Ayalabe, Kata ya Ganako ambayo ilitolewa kinyemela kwa mtu binafsi. Hadi leo ni takribani miezi minne eneo hilo bado halijarudishwa kwa umma;

Je, nini kauli ya Wizara kwa Kamishna wa Ardhi Kanda ya Kaskazini ili kutekeleza agizo hilo la Waziri ambalo wananchi walilishangilia sana? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza amezungumzia kwamba gharama za upimaji ni kubwa na hivyo wananchi wengi wanashindwa kulipa na wakati mwingine wanakuwa wako kundi kubwa wanaopimiwa. Naomba tu nimkumbushe Mheshimiwa Mbunge ya kwamba gharama za upimaji zimepunguzwa sana katika kipindi hiki cha miaka mitatu na huu mwaka wa nne tumeanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukikumbuka wakati tunaanza mwaka 2015/2016, gharama za upimaji zilikuwa juu sana zilikuwa wanachaji kwa ekari moja shilingi 300,000. Premium ilikuwa asilimia 15, ikapunguzwa ikawa asilimia 7.5 mwaka wa fedha uliofuatia. Kama hiyo haitoshi mwaka wa fedha uliofuatia 2017/2018 ikapunguzwa ikawa asilimia 2.5 na sasa hivi imepunguzwa ikawa asilimia moja. Maana yake ni kwamba zinakwenda zinapungua kutegemeana pia na uhitaji kama walivyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tukumbuke hapa katikati tumekuwa na zoezi kubwa la urasimishaji ambalo limechangia katika kupima maeneo mengi sana. Wakati wanaanza gharama zilikuwa kubwa, zilikuwa kwenye kama 250,000 mpaka 300,000 lakini kwa sasa kuna watu wanapimiwa kiwanja kwa shilingi 60,000; kuna watu wanapimiwa kwa 150,000; kuna watu wanapimiwa kwa 90,000, mifano tunayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Halmashauri ya Chemba nadhani wako kwenye 90,000; ukienda kwenye Halmashauri ya Mkinga wako kwenye 90,000; kwa hiyo zinakwenda zinashuka pia kutegemeana na uhitaji wa watu, kadri unavyokuwa na volume kubwa ya kazi na bei inapungua. Maeneo mengi sasa hivi yamepimwa kwa njia ya urasimishaji lakini katika kaya zinazopimwa kwa taratibu za kawaida gharama bado siyo kubwa kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amelalamikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili amezungumzia kufutwa kwa hatimiliki katika eneo la shamba moja katika Eneo Lake. Naomba niseme Mheshimiwa Waziri kutamka kwamba hati hiyo ifutwe ni jambo moja, lakini jambo la pili ni process pia kuhakikisha inafutwa na umiliki wake unaanza tena upya kwa namna itakavyokuwa. Unapofuta zile hatimiliki haina maana kwamba basi hapo hapo wanaanza kugawiwa, kuna utaratibu ambao lazima Mheshimiwa Rais aidhinishe na ikiidhinishwa inarudi kwa halmashauri husika na kuwekewa mpango maalum kwa ajili ya matumizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, haufutwi tu ukaletwa kwa wananchi moja kwa moja, unakuwa pia na maelekezo ya namna ya kupanga matumizi kutegemeana na mahitaji yalipo. Kwa hiyo, naomba nikuhakikishie tu kwamba ahadi iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri iko pale pale na muda utakapokamilika basi tutawaletea utaratibu wa matumizi mtakayokuwa mmejiandalia.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, katika kata husika nilizozitaja katika swali langu la msingi kuna baadhi ya mashamba wawekezaji wamehifadhi mapori ambayo hawayaendelezi. Mapori hayo yanahifadhi pia wanyama ambao ni hatarishi kwa wakati katika maeneo hayo.

Je, Serikali sasa wako tayari kwa kushirikiana na halmashauri kwa sababu, imekuwa ni changamoto ya muda mrefu, kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Karatu kuhakikisha wanayatambua haya maeneo na kufanya partial revocation na yale maeneo yarudi kwa wananchi ili wananchi wanaozunguka maeneo hayo pamoja na wanafunzi wanaoenda shule waishi katika maeneo salama bila kuathiriwa na maisha yao?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika mashamba hayo hayo niliyoyataja, kuna shamba mojawapo linaitwa Shamba la Benduu, mwekezaji alishafariki, nitamwandikia Mheshimiwa vizuri kwa karatasi; mwekezaji alishafariki, lile shamba wafanyakazi wake hawajalipwa takribani miezi nane na hawaruhusiwi kwenda kufanya kibarua kwenye mashamba mengine, hawajui hatima ya haya maslahi yao na hawajui hatima ya nini wafanye kwa sababu, wakitoka kwenda kufanya kazi kwenye shamba lingine anafukuzwa asirudi kwenye lile shamba. Je, sasa Serikali wako tayari kwenda kutatua mgogoro uliopo katika shamba hilo, ili wananchi wanaofanya kazi na vibarua wanaofanya kazi katika eneo hilo wapate haki zao na pia waruhusiwe kufanya kazi katika maeneo mengine, ili waendelee kujipatia kipato? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Paresso, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ameongelea kwamba, baadhi ya mashamba yamefanywa mapori na yanafuga wanyama kule ambao pengine ni hatarishi kwa watu na anaomba pengine yaweze kufanyiwa partial revocation kwa maana ya kwamba, ile sehemu ambayo pengine haitumiki basi iweze kuondolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, siwezi kutoa jibu la moja kwa moja kwa sababu, ni mpaka anachokisema hicho kiwe na uhakika kwa sababu, unapopewa shamba kuna muda wake wa kuweza kuliendeleza, ndani ya miaka mitano unatakiwa kuwa umeendeleza angalau moja ya nane ya hilo shamba. Sasa kama mashamba hayo hayajaendelezwa kwa kiwango hicho kwa sababu, tumeshasema uhakiki unaendelea kufanyika basi, tutapita pia kuona hilo shamba likoje, lakini kama nilivyosema mwanzo mashamba yote 25 ya Wilaya ya Karatu yamefanyiwa uhakiki na kwa sehemu kubwa yameendelezwa zaidi ya asilimia 50.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili anaongelea Shamba la Benduu, nadhani atanipa karatasi, kwamba, mwekezaji alikwishafariki na watumishi wale wanadai hawana malipo. Nadhani hili ni suala la kisheria zaidi kwa sababu, kama mtu amefariki kuna mtu ambaye anatakiwa kuwa administrator wa mali ya yule aliyefariki. Kama atakuwa ameteuliwa msimamizi wa mirathi katika eneo lile basi, huyo atabeba dhamana pia ya kuweza kulipa wafanyakazi ambao wanadai, wanayemdai alishafariki na tayari kuna mtu ambaye anasimamia mirathi ile atashughulikanao katika suala zima la kuweza kupata haki zao.
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ifahamike kwamba kuhusu upimaji wa ardhi ndani ya nchi yetu mlolongo huu umekuwa na kigugumizi kikubwa na kupelekea Serikali kupoteza mapato, migogoro ya ardhi isiyokuwa na lazima na tatu wananchi kukosa dhamana ya kwenda kuchukua mikopo maana yake wananchi kupata umaskini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu la kwanza; Ni lini Serikali itaweka utaratibu maalum wa kupima maeneo yote ambayo hayajapimwa kwa sababu Waziri alisimama kwenye vyombo vya habari akajinasibu akasema ndani ya mwezi mmoja mtu akishapimiwa atapata hati. Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu maalum wa kupima maeneo yote ambayo hayajapimwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa wananchi wa Basihaya wako tayari baada ya kukaa na Mwekezaji, Serikali na wananchi wa Basihaya wako tayari kulipa premium, kiwango ambacho kilikuwa ni makubaliano kati yao na premium ni kati ya 1% mpaka 1.5%. Ni lini sasa Serikali itakwenda kutoa hati katika maeneo hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Felista Deogratius Njau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ameuliza ni lini sasa Serikali itapima maeneo yote ili kuweza kuondoa pengine adha ambayo watu wanaipata. Naomba niseme tu bajeti ambayo tunaendelea nayo imeainisha namna ambavyo Wizara imejipanga katika kuhakikisha kwamba maeneo yote nchini yanapimwa. Katika kufanya hilo pia tumeweza kushirikisha makampuni binafsi katika kufanya ule urasimishaji kwenye yale maeneo ambayo tayari yalikuwa yameshakaguliwa. Suala la kupima nchi nzima liko katika utaratibu wa bajeti ya Serikali na inategemea pia na upatikanaji wa fedha, lakini mpango upo ambao tutakwenda kukamilisha upimaji. Hili pia linahitaji ushirikiano na taasisi binafsi ambazo tumekuwa tukizishirikisha ambapo nyingi zimeonekana pia hazina uwezo wa kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo kama Wizara tunatafakari namna bora ya kuweza kukamilisha zoezi hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ambalo amezungumzia habari ya umilikishaji katika maeneo yale, kwanza nataka tu niseme kwamba Mheshimiwa Felista anatakiwa kuishukuru sana Serikali kwa sababu maeneo yale ambayo anaombea watu kumilikishwa kisheria ilikuwa waondolewe, kwa sababu walikuwa wamevamia, lakini busara ya Wizara au ya Serikali ilipelekea kufanya mazungumzo ili wale watu waweze kumilikishwa na zoezi hilo linaendelea. Katika urasimishaji ile premium ambayo anaizungumza ni asilimia moja ambayo ni ya chini kabisa ukilinganisha na maeneo mengine ambayo wanalipa almost 2.5% na kabla ya hapo ilikuwa 15%, ikashuka ikawa 7.5%, ikaja 2.5% kwenye urasimishaji ni 1%. Kwa hiyo wanachajiwa kiasi cha chini kabisa kuweza kuwawezesha kupata umiliki.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la Hati, nadhani ninyi wenyewe ni mashahidi, Mheshimiwa Waziri pia ameweza kukaa ofisini na kuweza kuwapigia watu mmoja mmoja kuja kuchukua hati zao. Nimezunguka almost nchi nzima nikienda kugawa hati katika maeneo mbalimbali. Kuna hati ziko tayari lakini Watanzania hawaji kuchukua hati zao, lakini ukija nje wanasema hati hazitoki. Kasi ya utoaji hati kama tulivyosema ni ile ile ndani ya mwezi mmoja kama halmashauri imekamilisha taarifa zote, hati yako unaipata na zoezi hilo linafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Watanzania wale wote wanaohitaji kupata umiliki wa ardhi kama ambavyo ameongelea Mheshimiwa basi wawe tayari, pia ukishapeleka maombi yako uhakikishe umekwenda mpaka mwisho na umechukua hati yako. Wizara ndiyo custodian wa hati.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ardhi, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa vile Wizara ya Ardhi kupitia Tume ya Mipango ya Ardhi inasimamia na kuratibu shughuli za matumizi bora ya ardhi; na kutokana na kwamba Tume hii imeshafanya matumizi bora ya ardhi kwenye hatua tofauti tofauti, lakini maeneo mengi nchini hayajafikishwa kwenye hatua ya mwisho na hivyo kuwachanganya wananchi kwamba, matumizi bora ya ardhi yaanze kutumika au yasitumike: Je, ni nini kauli ya Serikali juu ya kukamilisha matumizi bora ya ardhi kwenye maeneo ambayo wamekwishaanza kuyapanga sasa?

Swali la pili; inaonekana wazi kwamba Wizara inahamasisha Halmashauri zitenge fedha: kwa kuwa Tume hii ambayo sasa inaonekana wanaendelea na huku Wizara inahamasisha tu; na kuhamasisha siyo kumlazimisha mtu, inakuwa siyo wajibu, yaani Halmashauri haiwajibiki moja kwa moja: Je, Serikali haioni kwamba sasa itoe nyaraka ambayo inaweza kuifanya kila Halmashauri itenge fedha hizi kila mwaka kwa ajili ya kutenga matumizi bora ya ardhi katika maeneo waliyonayo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza Mheshimiwa Tumaini anasema: Je, Wizara haioni umuhimu wa kukamilisha mpango wa matumizi katika yale maeneo ambayo yamekwishaanza?

Mheshimiwa Spika, ni kweli swali lake ni la msingi. Changamoto tunayoipata ni kwamba katika suala zima la uanzishwaji maeneo mapya, unaweza ukawa na kijiji ambacho tayari kilishafanyiwa mpango wa matumizi na wakaanza kuutumia, lakini baadaye tunapogawa maeneo unakuta tena kile kijiji kinakatwa. Kwa hiyo, ule utekelezaji wa ile mipango ya awali inashindikana kufanyika, inabidi kuanza upya.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai tu kwa Halmashauri zote nchini ambazo ndiyo mamlaka za upangaji, pale ambapo vijiji tayari vinakuwa vimeshawekewa mpango wa matumizi, tunaomba sana sana sana visifanyiwe mgawanyiko wowote. Kwa sababu, kitendo cha kugawanya kijiji kile kinaharibu mpango mzima, inabidi kuanza upya. Kwa hiyo, tumejikuta kuna vijiji tayari vilishafanyiwa mpango, lakini matumizi yake sasa yanashindikana kwa sababu kumezaliwa kijiji kingine ndani ya kijiji kingine. Kwa hiyo, naomba hilo liangaliwe katika Mamlaka zetu za Upangaji, nasi Wizara tutakuwa makini katika kufanya ufuatiliaji wa karibu.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anauliza kuhusu kuzitaka Halmashauri zitenge bajeti; pengine wanajivutavuta katika suala hilo, lakini nataka nimtie tu shime kwamba Wizara haijanyamaza katika hilo. Katika mwaka huu wa fedha tumetenga shilingi 1,500,000,000/=, kwa ajili ya kusaidia katika shughuli hiyo ya upangaji wa matumizi, lakini hii haiondolei Mamlaka husika za Upangaji kutotimiza wajibu wake. Kwa hiyo, bado tunasisitiza kila Halmashauri ya Wilaya ihakikishe katika vitengo vyake, inapopanga bajeti za maendeleo, waikumbuke sekta ya ardhi kuitengea bajeti ya kutosha. Kwa sababu ardhi usipoipangia matumizi ndiko huko ambako migogoro inaanzia.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara tunaingia katikati kuweza kusukuma hili jukumu liende, kwa sababu tunasimamia miongozo na nyaraka mbalimbali ambazo zinasukuma uendelezaji wa sekta ya ardhi. Kwa hiyo, ninachotaka au tunachoelekeza, Halmashauri zenye mamlaka, hili ni jukumu lao la msingi kuhakikisha upangaji, upimaji na umilikishaji unafanyika, kuhakikisha vijiji vyote vinakuwa na mpango wa matumizi ya ardhi, kwa kutenga bajeti stahiki na Wizara tutakuwa tayari kuendelea kuwasaidia. Kama ambavyo sasa hivi tunatoa fedha kwa ajili ya kupanga, kupima na kumilikisha katika maeneo yote.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa ridhaa yako unipe nafasi tu kidogo niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba Wizara imeweka mikakati, mbali na mpango wa matumizi ya ardhi katika maeneo ya vijiji, sasa tunakwenda kufanya zoezi la urasimishaji kwa nchi nzima. Zoezi hili litafanyika kwa nchi nzima bila kuacha mtaa wowote, tukisaidiana na wenzetu wa benki ambao watakwenda kutoa mikopo kwa mtu mmoja mmoja kuanzia kwenye kupima mpaka kumilikishwa. Mwananchi atakabidhiwa hati yake baada ya kuwa amemaliza kulipa mkopo. Mikopo siyo mikubwa kwa viwanja vya urasimishaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana tutakapokuwa tunaendelea kuhamasisha kwenye Halmashauri zetu, kwenye Wilaya zetu, tulipe kipaumbele ili tuwawezeshe wananchi wetu. Mheshimiwa Rais amesharidhia zoezi hilo lifanyike na tayari makubaliano na NMB Benki, Wizara imeshaingia nao. Tumeshaanza kama pilot area eneo la Mbarali. Kwa hiyo, tutafuata wapi, ni jitihada za Halmashauri wenyewe kuweza kuwawezesha. Ahsante.
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nilikuwa naomba Serikali itoe kauli, hasa kwa kutumia Sheria Na. 5 ambako halmashauri nyingi zipo huko kupima ardhi kwa kutumia hati za kimila; kwa sababu ukiangalia kwenye statement nyingi za halmashauri zetu inaonekana hoja kubwa ya migogoro ni kutokuwa na hati za kumiliki ardhi.

Je, Serikali ina mpango gani kwa kutumia hati miliki za kimila kuhakikisha maeneo yote ya umma, shule na vituo vya afya yanapimwa kama inavyotakiwa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa; ya kwamba hoja yake ni ya msingi na ni nzuri, lakini, shule ambazo zinamilikiwa na halmashauri haziwezi kupimwa kwa hati ya kimila, zile zinapimwa chini ya Sheria Na. 4; kwa maana ya kwenda kwenye general land. Kwa hiyo kama hitaji hilo lipo ni kwamba ni halmashauri pia, tuone namna ya kuhakikisha, na Wizara ilishaelekeza, kwamba taasisi zote za umma zipimwe. Huwezi kuipima kwa kutumia Sheria Na. 4.

Mheshimiwa Spika, niombe tu kwamba halmashauri zijipange katika kutumia Sheria Na. 5 kwasababu ile imeshaingia kwenye general land na haiwezekani tena kukaribisha kwenye umiliki wa kijiji. (Makofi)

SPIKA: Kwa hiyo Mheshimiwa Naibu Waziri zikishapimwa zitapewa hati each na hati ile inalipiwa kodi ya ardhi, au inakuwaje?

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, watapewa, na kodi inayolipwa sasa hivi; tulibadilisha sheria hapa mwaka 2019, wanalipa token tu, shilingi 5,000 kwa mwaka badala ya kutumia ukubwa wa eneo. (Makofi)
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na maeneo ya umma kama ambavyo Serikali imeelekeza na kuzielekeza halmashauri kupima lakini migogoro mingine mingi tunapata sana kwenye taasisi kama Majeshi na Magereza. Kwa mfano, Iringa pale Kata ya Isakalilo ina mgogoro mkubwa wa ardhi wa mipaka pamoja na wananchi na Jeshi la Magereza.

Je, Serikali inahusiana vipi na Wizara nyingine kuhakikisha pia inatatua hilo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, pia nimshukuru na muuliza swali.

Mheshimiwa Spika, Wizara katika zoezi zima la utatuzi wa migogoro kila tunapokwenda kwenye zoezi la migogoro utatuzi wake tunashirikisha halmashauri husika na tunashirikisha pande zote mbili. Na unapotaka kutatua mgogoro lazima uwe na lile Gazeti la Serikali linalotangaza mipaka ya eneo husika; na hauwezi kuutatua mgogoro ule unless mmekwenda kwenye site na kuweza kutafsiri. Kwa hiyo kazi kama Wizara tunayoifanya katika migogoro hiyo ya taasisi na wananchi tunaendelea kuitatua kwa kuzingatia sheria zinasema nini na mara nyingi tunapokwenda, Halmashauri husika inahusishwa na pande mbili zinazogombana zinahusika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama Kata ya Isakalilo na Magereza bado kuna mgogoro naelekeza wapimaji wa Mkoa wa Iringa wafike kule site ili waone namna ya kutafsiri mpaka ili kuondoa mgogoro huo.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kuongeza maswali ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nini tamko la Serikali kutokana na wawekezaji hawa wakati mwingine kujichukulia sheria mkononi na kuwafungulia watu kesi na kuwaweka ndani ikiwa hata wao hawafuati Sheria ya Ardhi, ikiwa ni pamoja na kuwa na hati sahihi, kuendeleza maeneo yale pamoja na kulipa kodi ya ardhi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni lini Wizara ya Ardhi itaingilia kati usimamizi bora wa matumizi ya ardhi ili kuepusha migogoro kati ya wakulima na wafugaji ambayo inaendelea kushika kasi ndani ya Jimbo la Momba?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Condester.

Mheshimiwa Spika, napenda tu nimhakikishie; kwenye swali lake la kwanza anataka kujua nini tamko la Serikali kwa hawa wawekezaji ambao wanajichukulia sheria mkononi.

Mheshimiwa Spika, kwanza nitoe rai tu kwa wananchi kuhusu namna ya uuzaji wa ardhi kwa wawekezaji. Tuwaombe sana, kwa sababu mara nyingi wawekezaji wanaenda moja kwa moja kwenye maeneo, wanaonana na watu bila kufuata taratibu na wanauziana bila kuzingatia sheria; na hatima yake anapokuwa amepewa hati yake wewe ulimuuzia hekari 100, anakuja na hati yenye hekari zaidi ya 100, ni kutokana na nyaraka ambazo zinatakiwa kuwepo kwa kuzingatia sheria yenyewe.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi niwaombe, kwanza nitoe rai, kwamba, ili kuondoa hii migogoro uuzwaji wowote wa ardhi lazima uhusishe halmashauri husika ambao ndio wanaotambua mipaka yako na namna ambavyo mnaweza kuuziana ardhi kwa wawekezaji. Na wakati mwingine unaweza ukamuuzia mtu ambaye hata si raia wa Tanzania ilhali hairuhusiwi kwa raia wa kigeni kuweza kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Spika, kwa suala la kodi ambazo hawalipi, tayari tulishaanza mkakati wa kuwafuatilia. Tunachohitaji tu ni halmashauri husika kuona ni namna gani pia ya kuanza ule mchakato wa kufuata sheria, taratibu zile za kutoa maonyo kuanzia kwenye Kifungu cha 45 mpaka 48 ambavyo vinaelekeza njia nzuri ya kuweza kumnyang’anya mtu hati yake hata kama amepewaa kisheria.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, anasema ni lini Wizara itaingilia kati ili kumaliza migogoro hii ya wakulima na wafugaji. Tatizo hilo linaweza likaisha pale tu ambapo kijiji kitakuwa na mpango wa matumizi ya ardhi; na matumizi ya ardhi hayapangwi na Wizara, yanapangwa na maeneo husika. Kwa hiyo sisi kama Wizara intervention yetu inakuja pale ambapo tunakuja sasa kuridhia kile ambacho mnakubaliana katika kutenga maeneo. Kwamba wafugaji wanatengewa maeneo yao, wakulima maeneo yao, maeneo ya makazi nayo yanakuwepo. Kwa hiyo tunapokwenda sisi ni kuweka ile mipaka kwa ajili ya kuheshimu taratibu hizo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama vijiji hivi havijawa na mpango wa matumizi basi tunaielekeza pia Tume ya Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi ikashirikiane na Wilaya ya Momba waweze kuweka matumizi ya ardhi katika maeneo yenye mgogoro. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona, tatizo lililoko kule Momba linafanana sana na kule Arumeru Mashariki maeneo ya Kia kwenye mashamba ya Malula. Wakulima wa eneo lile walipewa notice na Serikali kwamba wataondolewa lakini wangefidiwa. Hata hivyo, kabla ya zoezi hilo kufanyika kukazuka mgogoro na wawekezaji hawajaonekana pia Serikali inasema kwamba wakulima wale wako pale kimakosa na mashamba yale yalikuwa ni ya Serikali. Je, ni lini Serikali itatoa tamko kuhusu wakulima wale kwamba watafidiwa au la au wataendelea na kufanya kazi zao za kilimo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika maeneo ambayo kumekuwa na migogoro kati ya wawekezaji na wananchi maeneo mengi ambayo yana migogoro ni yale ambayo wawekezaji walipewa na wakayatelekeza mashamba yao matokeo yake wananchi wakawa wameingilia pale. Kisheria ni kwamba kama mtu amekaa pale kwa muda wa miaka 12 bila kusumbuliwa anakuwa na uhalali wa kuendelea kumiliki eneo lile kama katikati hapakuwa na mawasiliano ya kuweza kujua kwamba anadai eneo lake limevamiwa au namna gani. Sasa pale kama Serikali ilishaingia na kuwatambua kwamba wananchi wana haki basi hilo kwa sababu ndio nimelipata hapa, naomba nilichukue ili nifanye ufuatiliaji wa karibu kuweza kujua uhalisia wa kile anachokisema na hali halisi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kuzungumzia katika maswali haya hasa katika mashamba yaliyotelekezwa ni jukumu pia la mamlaka zenyewe za upangaji kufanya ufuatiliaji kuweza kufanya ukaguzi kuona mashamba yote yale ambayo yanamilikiwa na wawekezaji au hata kama ni mtu binafsi lakini amelitelekeza kwa maana ya kukiuka masharti yaliyoko kwenye hati yake, utaratibu wa kuanza kutaka kumnyanganya unaanzia kwenu kama halmashauri.

Kwa hiyo, wakishaleta sisi kazi ya Waziri ni kumshauri Mheshimiwa Rais kufuta pale ambapo anakuwa amekizi vigezo. Kwa hiyo, nitoe rai kwa halmashauri zote kule kuliko na mashamba pori ni jukumu la halmashauri sasa kuanza kufanya ufuatiliaji, ku-save notice, kutoa maonyo na mwisho wa siku wakipendekeza kufutwa Wizara itakuwa tayari kushirikiana nao kuhakikisha taratibu zinafuatwa, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza; kwa kuwa eneo lote lile la mlima lilikuwa la kijiji na kwa kuwa sheria zetu za ardhi haziruhusu mtu kwenda kuvamia kijiji au Kamati ya Ulinzi kwenda kutwaa eneo la kijiji na kuligawia taasisi nyingine, ile ni mali ya wanakijiji.

Sasa ni lini taasisi hiyo iliyotwaa eneo la wanakijiji watalipa fidia ya kaya 10 ambazo zilikuwa zinafanya kazi pale? Hilo swali la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa migogoro ya ardhi Mkoa wa Mara imekuwa mingi sana na hata juzi tumesikia Rorya pale kuna mtu amekufa kwa migogoro ya ardhi. Ni lini sasa Serikali itaenda kupima hasa vijiji 30 vya Tarafa ya Chamriho, Jimbo la Bunda kuwapa Hati ya Kimila?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Getere kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza Sheria ya National Environmental Management Act No. 20 ya 2004 hairuhusu maeneo yale ambayo ni hatarishi kama milima na maeneo ya kingo za mito kuweza kumilikiwa na wananchi, yanakuwa ni protected chini ya usimamizi wa Waziri wa Ardhi. Kwa hiyo, eneo la mlima analolizungumzia si halali kwa watu kumilikishwa pale na litabaki under protection kama ambavyo Kamati ya Usalama ya Wilaya imekwishaelekeza kuwapa watu wa Magereza kuliangalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusiana na vijiji 30 kuhusu suala zima la kuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi; kama nilivyojibu juzi, ni suala tu la mamlaka yenyewe ya upangaji, pale watakapokuwa tayari sisi kama Wizara kupitia Tume ya Mpango wa Matumizi ya Ardhi tutakuwa tayari kushirikiana nao kwa sababu kadri wanavyopima na kuweka mpango wa matumizi katika vijiji vyao, ndivyo jinsi ambavyo wanapunguza migogoro ya ardhi kwa watumiaji ardhi katika maeneo. Kwa hiyo, sisi tupo tayari wakati wowote pale ambapo Halmashauri itakuwa tayari kufanya kazi hiyo, waangalie kama bajeti wanayo, tutakwenda kuwasaidia, ahsante.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nilipata fursa ndani ya kipindi cha mwezi mmoja uliopita nilienda kutembelea eneo hilo na bahati nzuri tulikuwa na Mbunge husika na zile kaya tuliweza kuzibaini pale katika eneo lile. Tulichokifanya na Kamati ya Ulinzi na Usalama chini ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya tukasema kwamba wale ambao kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira maana yake hakuna compensation isipokuwa nini utaratibu wa busara ufanyike.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, jambo hilo tumeliacha chini ya Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, DC wetu wa Tarime linafanyiwa kazi lakini utaratibu wa kulitangaza eneo lile kuwa eneo lindwa, utaratibu huo kwa mujibu wa Kanuni zetu tunaenda kubadilisha Kanuni hivi sasa si muda mrefu tutatangaza baadhi ya maeneo likiwemo eneo la Mlima Nkongore, ahsante sana.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kitu cha kwanza, majibu niliyopewa ni tofauti kabisa na majibu ambayo nimesomewa na Waziri, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sheria inasema, wakithamini wanapaswa walipe wale wathaminiwa ndani ya miezi sita; na kwa kuwa watu wengine wameshalipwa: Je, wale ambao hawajalipwa, kuna nyongeza yoyote ambayo itawekwa kwa ajili ya fidia kwa sababu Serikali imechelewa kulipa na hawajaweza kuendeleza maeneo yao? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili: mwananchi yeyote anapochukua kiwanja cha Serikali ambacho kimepimwa anakuwa amejihakikishia makazi yake kwa sababu atajiandaa katika maisha yake; kuchukua viwanja vyao, ukachelewa kulipa ni kuwadumaza: Pamoja na majibu aliyotoa, wale watu waliobaki watalipwa lini kwa commitment ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Conchesta kama alivyouliza. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Dugange kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ana hofu ya kujua kwamba wale ambao hawajalipwa, watalipwaje pesa zao? Je, kutakuwa na nyongeza? Sheria iko wazi na tuliipitisha hapa 2019 tukafanya marekebisho kwamba inapofika miezi sita kama hajalipwa, tunaanza ku-calculate interest kwa bei ya soko iliyopo wakati huo. Hii inakwenda ndani ya miaka miwili, ikifika miaka miwili hawajalipwa maana yake lile zoezi inabidi lianze tena uthamini upya. Sheria tuliipitisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe hofu tu kwamba watu hawa watalipwa kwa bei ya soko wakiwa wamewekewa na riba yao katika pesa walizochukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anauliza, ni lini pengine wataacha kuchukua maeneo ya watu halafu wanakuwa hawana uhakika wa malipo yao? Naomba niseme tu kwamba katika maeneo ambayo Serikali inakuwa na interest nayo, lazima itaongea na washirika waliopo pale, wenye ardhi zao, kuwaambia dhamira na nia njema ya Serikali; na kabla ya kutwaa kunakuwa na makubaliano ambayo ni lini maeneo haya yatatwaliwa na kwa kazi ipi? Inapokuwa na public interest, huwa haina majadiliano zaidi ya kukaa nao na kukubaliana nini kifanyike?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa hili ambalo tayari tunaona ni miradi mikubwa ya Kiserikali ambayo inapita, hatutakuwa na mjadala mwingine isipokuwa ni kuzungumza nao. Tayari Tume ya Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi katika maeneo yote inayopita miradi mikubwa, wameshaandaa mpango wa matumizi ya ardhi. Kwa hiyo, wale watakaobaki pale, watapimiwa maeneo yao, wale watakaotakiwa kuondoka kwa ajili ya kupisha pengine labda ni zile stations zinazojengwa, basi watapewa fidia yao kwa mujibu wa soko la wakati huo. (Makofi)
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa umilikaji halali wa ardhi utaisaidia Serikali katika kukusanya mapato kwa sababu wamiliki halali watalipa kodi vizuri na kwa kuwa kwa uzoefu uliooneshwa kutokana na shida ya uhamishaji wa umiliki unaonesha kwamba wananchi wa kawaida wanashindwa kumudu gharama. Je, Serikali iko tayari ikiwezekana kufuta kabisa gharama za kuhamisha umiliki ili wamiliki waweze kumiliki na kulipa kodi kwa Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Rais hayati Dkt. John Pombe Magufuli kwa maombi ya wananchi wa Mtama walifuta umiliki wa shamba la Maumbika lililoko Jimboni Mtama na kulikabidhi kwetu, lakini tukiwa katika utaratibu wa kuligawa kwa wananchi, Serikali hiyo hiyo ili-reverse uamuzi wake. Je, Serikali iko tayari sasa kutumilikisha shamba hili ili wananchi waweze kulitumia kwa sababu limetelekezwa kwa muda mrefu na mmiliki wa shamba hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nape, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka tu nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali hii ni sikivu na kila mara wananchi wanapotoa kilio chao, Serikali hukaa na kuanza kuangalia upya kuweza kuona ni jinsi gani tunaweza kuwasaidia. Kwa hiyo katika suala zima la kusema kwamba pengine gharama ya uhamishaji miliki iweze kufutwa ili watu waweze kumiliki wengi bila tatizo lolote, naomba niseme tu Serikali hii inaendeshwa kwa kodi za wananchi. Sasa ukishaanza kuzifuta kodi ambazo pengine ni ndogo na ni token ukiziangalia, mwisho wa siku utakuta Serikali haina njia nyingine yoyote ya kupata mapato na kujikuta kwamba tunakwama. Tunachofanya kama Serikali ni kuendelea kupunguza zile kodi ambazo pengine zina kelele.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, nikizungumzia suala la muuliza swali ambaye aliuliza swali la msingi, Mheshimiwa Stella Manyanya kwenye eneo lake hata zile tozo wanazotoza katika masuala mazima ya ardhi ziko chini sana. Ukiangalia kwenye makazi walikuwa wanatozwa shilingi 15 lakini sasa hivi wanatozwa shilingi 11 ambazo ni kidogo sana. Kwenye maeneo ya biashara ilikuwa shilingi 30, sasa hivi wanatozwa shilingi 21, hata shilingi 100 haijafika. Ni ndogo ndogo ambazo wananchi wakiweza kulipa kwa hiari ni pesa ambazo unaweza ukazikusanya na zikafanya kazi kubwa katika Taifa hili. Kwa sababu wazo limetolewa, naomba tulipokee na sitaweza kulitolea maamuzi sasa hivi kwa sababu ni lazima mchakato uweze kupita.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ameongelea suala la shamba la Maumbika kwamba Serikali ilifuta umiliki wake kwa kushindwa kulimiliki halafu baadaye pengine maamuzi yakabadilika. Naomba niseme kwamba, wakati mwingine tunapotoa ilani kwa ajili ya kubatilisha milki za watu, tunaangalia hatua iliyofikiwa lakini halmashauri husika ndiyo inayoleta notice au maombi yake kwa Waziri kuomba shamba lile lifutwe kwa sababu wameshindwa kutimiza masharti lakini wakati huo wanakuwa wamempa notice ya siku 90 ili aweze pengine kujitetea kwamba kwa nini hakuweza kumudu au kufuata masharti yale yaliyowekwa. Kwa hiyo utetezi unapokuwa wakati mwingine una uhalali na mantiki ndani yake, Serikali pia huwa inabadili mtazamo wake na kuweza kumrudishia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa suala hili la Maumbika ambalo amelizungumza lazima kuna kitu ambacho kilikuwa kimetokea katika hilo kwa sababu sikuweza kuliangalia kwa undani wake kuweza kujua ndiyo amelitoa sasa hivi. Basi kama lina maelezo ya ziada zaidi ya hizi taratibu za kisheria, niko tayari kumjibu baadaye. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana na ya uhakika ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nataka tu kuwafahamisha Waheshimiwa Wabunge kwamba nchi hii kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi, Na. 5 Ardhi ya Vijiji na Na. 4 Ardhi ya Jumla tunatoa hati mbili. Kuna hati ambayo ndiyo hiyo inayosababisha wanyonge wananchi wanamiliki, tuna hati ya kimila ambayo inatolewa kwa mujibu wa sheria ambayo zaidi ya asilimia 90 ya hao wanyonge wa nchi hii wanapewa hati za kimila na ndizo zilizo nyingi kuliko hizi hati za mjini. Hawatozwi pesa ya kuanzia wala ada ya kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nataka niwaambie kwamba Serikali kupitia Bunge hili mlitunga sheria nzuri sana inayowatambua wanyonge. Wanyonge wote wanaomilikishwa zile ardhi wanazozitumia kwa shughuli zao za uzalishaji wa kila siku hawatozwi lolote, hawana kodi ya uhamishaji wala hawana kodi ile la land rent ya kila mwaka na hawana ukomo. Ana miliki leo, hana miaka 33 wala miaka 99 kama hati za mjini. Kwa hiyo suala la wananchi maskini wametambuliwa kwa mujibu wa sheria na waendelee. Hivi sasa Bunge lako halijawahi kutunga tozo yoyote kwa wananchi maskini wanaomiliki ardhi kwa mujibu wa sheria hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili la Maumbika, nalijua vizuri. Tulikuwa na makusudi ya kufuta na ni kweli yule mwekezaji ametelekeza lile shamba. Nataka uwaambie wananchi wa Jimbo lako la Mtama, leo nakupa ahadi, nitakapokuwa naosma bajeti hapa, nitakupa barua nataka lile shamba limilikiwe na Halmashauri ya Wilaya ya Mtama ili wananchi wa pale waliendeleze iwe sehemu ya mapato yao. Walime korosho kwa sababu lile shamba ni la korosho, mmiliki alilitelekeza siku nyingi, tuko kwenye hatua za mwisho za kuliondoa, lakini kwa sasa ningeomba watu wa halmashauri waendelee kuliangalia angalia, kama kuna korosho humo waanze kuokotaokota. Barua kamili ya umiliki wa shamba lile kurudi halmashauri nitaitoa hapa wakati nitakapokuwa nawasilisha bajeti yangu. (Makofi)
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi ya swali la nyongeza. Naomba kuuliza swali moja; Serikali imeweka mfumo wa kidigitali wa kulipa kodi za ardhi, lakini mfumo huo haumruhusu mwananchi kupata control number moja kwa moja, ni mpaka afike kwenye ofisi za ardhi ili kuhamasisha ulipaji kodi kwa haraka na kumwepushia mwananchi kulipa faini zisizo za lazima, je, Serikali haioni haja ya kuboresha mfumo huu ili kumwezesha mwananchi kulijua deni lake moja kwa moja kama wanavyofanya Wizara ya Maji? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanaisha kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna changamoto katika suala zima la kuweza kupata zile bill kupitia mtandao, lakini bado kama Wizara tulirahisisha kwa kutumia simu zetu ukipiga *152*00# unafuata maelekezo kama ambavyo tunafanya katika masuala ya M-Pesa na mambo mengine. Suala la msingi unalotakiwa kujua wakati unatafuta kujua bill yako unatakiwa uwe unajua plot number yako ya kiwanja au namba ya hati yako kwa sababu itakuuliza na wakati huo itakuuliza kama kiwanja chako kiko Dar es Salaam au kiko mikoani. Kwa Dar es Salaam unaweka namba moja (1) lakini kwa mikoani unaweka namba mbili (2) halafu unafuata maelekezo. Kwa hiyo kuna wakati mwingine mitandao inasumbua, kweli inakuwa ni shida lakini ukiweza kupata mahali ambapo mfumo umekaa vizuri, bado unaweza ukapata bill yako, unaweza ukalipa kodi yako kwa kutumia simu yako hiyo hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa kama Wizara pia tunajaribu kuboresha mifumo kwa sababu kuna wakati mwingine unadaiwa 500,000 una 300,000 unataka kulipa. Ule mfumo mara nyingi hauruhusu kulipa part payment, inabidi uwasiliane na Afisa Ardhi ili aweze kukupa. Sasa hivi wataalam wetu wanafanyia kazi hiyo ili uweze kulipa hata kama una sehemu ndogo ya kuweza kulipa basi utalipa part payment na nyingine utakuja kumalizia na mfumo utapokea na Wizara ndiyo kazi inayoifanya sasa hivi. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. naomba niulize maswali mawilinya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kijiji cha Jasini kwa Kata ya Moa na Mayomboni, Wilaya ya Mkinga wanapata usumbufu sana wa kukamatwa na askari wa Kenya na kwenda kushitakiwa Kenya na wakati mwingine mali zao kutaifishwa.

Je, ni lini sasa Serikali itahakikisha hali hii inakoma? Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili,...

SPIKA: Wanakamatwa kwa sababu gani?

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, wanaonekana wameingia Kenya, wakivua Kenya, ni eneo la bahari.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, askari wa Kenya mara kadhaa wanaingia Jasini, hali ambayo ni hatari sana kwa nchi zetu hizi mbili.

Je, ni lini sasa Serikali itachukua hatua za haraka za kuhakikisha inaweka mipaka ili kuhakikisha Serikali ya Kenya na Tanzania zisije zikaingia kwenye migogoro? Asante nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA
MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nikiri ni kweli katika eneo la Jasini kwenye Kata ya Moa na Mayombo mara nyingi kumekuwa kukitokea ukamataji wa wananchi wa eneo hilo na hili pia liliwahi kutokea wakati pia tuko ziara kule, nilishafika mpaka Jasini.

Mheshimiwa Spika, lakini kinachotokea hapa ni kutokana na kwamba katika uimarishaji wa mpaka tumesema tunaimarisha kwanza maeneo ya nchi kavu kwa sababu majini katika kuweka maboya tayari mpaka nchi zote mbili ziridhie wapi maboya yawekwe, pamoja na kwamba, tunajua kuna ule mbali wa nautical miles 200 ambazo ziko kwetu, lakini hii haijaweza kufanyika kutokana na hali halisi ambayo kila ukitaka kuweka alama lazima mkubaliane wote.

Mheshimiwa Spika, lakini napenda kushukuru sana Balozi zetu, Ubalozi wetu wa Kenya pamoja na ule mdogo wa Mombasa. Nimshukuru sana Mheshimiwa Pindi Chana wakati yuko pale wametatua matatizo mengi kutokana na kesi hizi na sasa hivi balozi aliyeko pale, Consular Athumani Haji aliyeko Mombasa, ni juzi toka miezi sita iliyopita wameweza kutatua pia changamoto hiyo ya kuweza kukamatwa.

Mheshimiwa Spika, tatizo lililopo kutokuwekwa kwa maboya pale ni kutokana na makubaliano ya nchi mbili, lazima mkubaliane ndio muweke alama hizo. Bila kukubaliana hakuna nchi itakayoweza kuweka.

Mheshimiwa Spika, na kingine ambacho ni changamoto kule sasahivi wameanzisha sheria ya uvuvi ambayo chombo kinapoingia ziwani lazima ulipe dola 500 na ukikamatwa pale fine ni dola 300. Sasa mara nyingi wavuvi wetu wanakuwa hawana, lakini diplomasia imekuwa ikitumika wanajadiliana kati ya ubalozi n akule na watu wanatoka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba katika swali lake la pili analosema ni lini hii itakomeshwa? Niwaombe tu muwe na Subira kwa sababu mchakato unaendelea katika suala zima la kuimarisha mipaka kama ambavyo nimesema katika jibu langu la msingi. Tukiimarisha mipaka hiyo ya nchi kavu ikikamilika suala la kuweka maboya ndilo limebaki kwa sababu tayari mpaka ulishabainishwa isipokuwa ni kuweka alama tu. Tutaweka mara tutakapokuwa tumekubaliana na wenzetu wa Kenya.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Wizara, ninaomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Manispaa ya Moshi ndiyo manispaa ndogo zaidi Tanzania yenye kilometa za mraba 58; na kwa kuwa upanuzi wa makazi na shughuli za kiuchumi ambazo zinasababisha ukuaji wa mji ule zinakwenda kugusa mamlaka za sehemu nyingine ambazo watendaji wa Wilaya ile hawana mamlaka nazo.

Nini nafasi ya Serikali katika kurasimisha maeneo hayo kabla ujenzi holela haujaendelea?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA
MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Manispaa ya Moshi ina eneo dogo, na katika kupanuka kwake inabidi iguse na maeneo mengine ambayo yako nje ya utawala wa Manispaa ya Moshi. Lakini taratibu za Serikali ziko wazi, pale ambapo maeneo ya utawala yanatakiwa kuongezwa ama kupunguzwa, taratibu lazima zifuatwe kupitia Wizara ya TAMISEMI ili kuweza kujua uhalali wa kuweza kuongeza eneo waweze kupata kama wanavyohitaji. Vinginevyo hawawezi kufanya zoezi katika eneo ambalo si la Manispaa, isipokuwa waliopo Moshi DC wanaweza wakafanya zoezi la urasimishaji na kupanga maeneo yao kutokana na sheria inayo…
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, napenda kuuliza:-

Mheshimiwa Spika, huko Nyakasangwe ambapo kule nyuma kumetokea mauaji kwa sababu ya matatizo ya ardhi. Je, ni lini sasa Waziri atakwenda pamoja nami huko ili tushughulike kuweka mambo ya wananchi sawa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, napenda nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge, Askofu Gwajima, kwamba tutapanga wakati wowote tuweze kwenda kwa sababu sasa tuko kwenye bajeti, lakini tutapata fursa nzuri ya kwenda kwenye eneo alilolitaja.
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Shirika la Nyumba la Taifa lengo lake kisheria ni kujenga nyumba za kupangisha na kuuza kwa wananchi wa kima cha chini na hii inasababisha wananchi wale kununua kwa bei rahisi. Hata hivyo, Shirika linashindwa kutekeleza jukumu hili kutokana na Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambayo inakuwa kwenye vifaa vya ujenzi. Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuondoa hii kodi katika vifaa vya ujenzi kwa shirika la nyumba la Taifa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Ripoti ya CAG ya 2019/2020 ilionesha kwamba mradi huu usipokamilika mapema basi Serikali itaingia hasara kwa kulipa Shirika la Nyumba shilingi bilioni 100 na mpaka sasa wakandarasi wanalipwa. Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kutekeleza mradi huu ili kuepuka hasara hii ya Taifa ambayo inaenda kuingia?

Mheshimiwa Spika, lakini pili, kuweza…

SPIKA: Aahaa, tayari maswali mawili. (Kicheko)

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa sababu muda hautoshi, nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge kwa sababu sheria ilipitishwa Bungeni humu aangalie malengo mazima ya uanzishwaji wa Shirika la Nyumba. Mbali na hilo alilolisema, lakini kwa sasa Shirika la Nyumba halipati ruzuku yoyote kutoka Serikalini na hivyo ni shirika linalojiendesha kibiashara. Kwa hiyo, katika miradi linayofanya kuna kujenga zile nyumba za gharama nafuu ambazo watu wananunua na wengine wanapanga, lakini pia linakuwa na miradi ya kibiashara ambayo inaliongezea pato Shirika ili kuweza kupanua miradi na kuweza kuongeza wigo wa kupata pesa kwa ajili ya kuendelea kujenga. Kama sasa hivi hapa Dodoma wana mradi wa nyumba 1,000 ambao wanaendelea kujenga nazo ziko katika viwango tofautitofauti.

Mheshimiwa Spika, ameongelea suala la kuondolewa kwa VAT kwa Shirika la Nyumba. Naomba niseme tu, katika suala zima la ujenzi ni mashirika mengi ambayo yanafanya kazi hizi za ujenzi ikiwemo Watumishi Housing. Kwa hiyo, unapozungumzia suala la kuondoa VAT, Watumishi Housing nao wanajenga nyumba kwa ajili ya wafanyakazi, sasa huwezi ukasema unaondoa VAT wakati haya mashirika yote yanafanya huduma ileile ya ujenzi wa nyumba kwa ajili ya kuboresha makazi kwa watu wetu. Kwa hiyo, hili kama linaonekana kwamba ni tatizo basi nadhani ni jambo la kuangaliwa upya, lakini kwa sasa bado VAT itaendelea kutozwa kama ambavyo inaendelea, japokuwa kama Wizara tulikuwa na mpango awali wa kuangalia namna bora ya kuweza kuliwezesha Shirika kwa kuangalia pia katika suala hilo la VAT, lakini bado mchakato haujafikia mwisho wake kwa sababu ya hali halisi ya ushindani na mashirika yanavyofanya kazi kama hiyo.

Mheshimiwa Spika, anaongelea suala la utekelezaji wa mradi ule kwamba unapata hasara na CAG ameonesha. Kwenye jibu langu la msingi nimesema ya kwamba kwa sasa tumepanga mradi huo utaendelea na ujenzi katika mwaka wa fedha huu 2020/2021 kwa sababu kubwa tu kwamba mradi wa Morocco Square ambao unaendelea mpaka sasa na tayari umefikia kwenye asilimia 92 ukikamilika ule tayari unaongeza vyanzo vya pesa kwa ajili ya ku-subsidize matumizi katika ujenzi ule. Pia tunayo Victoria Palace ambayo ina unit 88 lakini pale tayari 86 zimeshanunuliwa. Kwa maana hiyo ni pesa inayoingia kuliwezesha Shirika mbali na kutegemea mikopo basi pia kutoka katika vyanzo vya ndani vya miradi yake ya uwekezaji vitaenda kusaidia kuweza kukamilisha mradi ule ili kuweza kuboresha mji ule ambao uko katika eneo ambalo ni very prime.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninalo swali kidogo la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, kukamilika kwa Mji Mpya wa Kawe utaongeza shughuli za kijamii kwa wananchi wanaokaa kwenye eneo la Kawe, hasa Mzimuni, Ukwamani na maeneo mengine. Kukamilika kwa Mji Mpya wa Kawe ni kiashiria cha Kawe yetu ijayo kuwa wilaya. Je, ni lini hasa Mji Mpya wa Kawe utakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kumjibu Mheshimiwa Askofu Gwajima swali lake la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze kwa sababu baada ya kuingia tu Bungeni amekuwa akifuatilia sana mradi ule ili kuweza kuona unakamilika lini ili uweze kupendezesha maeneo yale. Azma ya Serikali hata ilipohamishia Makao Makuu hapa Mji wa Dar es Salaam ulibaki kama mji wa kibiashara. Kwa hiyo, lengo letu kama Serikali pia ni kuhakikisha kwamba mradi ule unakamilika ili ile maana halisi ya kufanya Dar-es-Salaam kuwa mji wa kibiashara na Kawe kuonekana kama satellite town ambayo tumekusudia kuifanya hivyo tumesema mwaka wa fedha unaokuja mradi ule utakwenda kukamilishwa. Kwa hiyo, asiwe na wasiwasi Mheshimiwa Wizara iko makini katika hilo. (Makofi)
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naishukuru Wizara kwa majibu haya. Swali la kwanza; kwa kuwa taratibu hizi za Ilani zimekwisha kukamilika na kwamba mmiliki huyu anatumia ardhi isivyo stahili. Je. Waziri anatuambia nini kwa kuwa taratibu hizi zimekamilika ni lini sasa hati ya mashamba haya zitafutwa baada ya kupelekwa kwa mamlaka ya Mheshimiwa Rais? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa barua ya mapendekezo ya kufuta hati ya shamba hili yalizungumzia vile vile Shamba la Mwele ambalo, Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja kutembelea Mkinga alitoa maagizo kwamba, ardhi ile imegwe kutoka kwenye shamba la Serikali kwa sababu, limetelekezwa kwa zaidi ya miaka 20. Je. Waziri yupo tayari kufuatilia jambo hili ndani ya Serikali ili agizo lile la Waziri Mkuu liweze kufanyiwa kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza amezungumzia kwamba taratibu zile zinazotakiwa kufuatwa katika ubatilishwaji zilishakamilika. Naomba kukiri ni kweli kwasababu barua ya ubatilisho ilitoka tarehe 10 Machi, 2020 maana yake kufikia Juni, 2020 tayari utaratibu ule ulikuwa umekwisha. Lakini wakati huo huo mmiliki huyu alileta utetezi wake akitetea kwamba asiweze kunyang’anywa kwasababu alizokuwa amezilieleza. Lakini baada ya kuangalia pia ilionekana kwamba miliki ile ilikuwa imewekezwa kama dhamana kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Lakini hiyo pia haituzuii kama wizara tumetoa maelekezo kwenye halmashauri kwasababu ile hati imeshawekwa dhamana katika Benki, na Benki yenyewe ni Benki ya Nje kwa hiyo tumeshaelekeza na tayari wamekwisha toa ilani kwa ajili ya kubatilisha tena wamempelekea na yule mmiliki wa Benki ili ajue kwamba dhamana aliyonayo kisheria kwa sheria za Tanzania sasa haitakiwi iwe kule kama ambavyo inapaswa.

Kwa hiyo, tunasubiri hizi siku zikiisha basi tutaweza kufanya kile ambacho kinatakiwa kufanywa kisheria na watu wa Halmashauri ya Mkinga wataweza kufaidika na lile shamba. Namuomba tu Mheshimiwa Mbunge basi awe na subira katika hilo kwasababu tayari taratibu zinafanyika na ilani imekwishatumwa kwenye ile Benki ya Nje pamoja na kwa mmiliki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Swali lake la pili anaongelea suala Mweru ambalo lilikuwa na maelekezo pia ya Waziri Mkuu. Kwanza nichukue fursa hii pia kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dunstan Kitandula kwasababu amekuwa akifuatilia sana. Nakumbuka hata mwaka jana, mwaka juzi kuna shamba la MOA alilipigia kelele taratatibu zilifuatwa likabatilishwa na wakaweza kupewa na sasa wananchi wanalitumia kwa mujibu wa waliyoelekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika hili naomba nimuhakikishie kwamba, tutachukua speed isiyo ya kawaida tunahakikisha kwamba tunafanya ufuatiliaji na kama umemsikia pia Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Sita amesema hana mzaha na wale ambao wana hodhi ardhi bila ya kuzitumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Na sisi kwa kasi ile ile tutaendelea mbali na hilo shamba la Mweru tutaangalia pia na mashamba mengine katika maeneo mengine ambayo wameyahodhi ili tuweze kuchukua hatua stahiki na yaweze kutumika kwa matumizi ambayo yataleta faida kwa wananchi lakini kwa Taifa kwa ujumla. Ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu yaliyotolewa na Serikali yanayoridhisha kwa wastani, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa, majibu ya Serikali yanaeleza wazi juu ya utoaji wa hati 845 tu kati ya upimaji uliokamilika wa watu 100,041 asilimia 0.0056 katika kipindi chote cha miaka miwili. Je, Serikali haioni sasa ni muda sahihi wa kupunguza lile tatizo la premium ambalo linasababisha bei kubwa kwa wananchi ambao wanashindwa zaidi ya ile 180,000 ambayo wamelipa kwa wale wa kampuni? Sasa hapa ni kupunguza ile premium.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; ni kweli kwenye majibu ya msingi inasema wachangiaji ni 30,000, lakini kwa taarifa nilizonazo kama Mbunge ni zaidi ya wachangiaji 80,000. Kwa hiyo, jumla ya fedha ni bilioni nne wanazisema, mimi nasema bilioni 15. Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kupeleka Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali ili akafanye ukaguzi maalum tuje na takwimu zilizo sahihi kwa ajili ya fedha za wananchi zilizopotea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu maswali yake mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mtemvu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nimsahihishe, si kweli kwamba, hati 847 tu ndio zimeandaliwa. Kwenye jibu langu la msingi nimesema hati 1,754 kati ya waombaji 1,925 tayari zimeandaliwa na wamechukua, lakini tunaendelea kuandaa hati kwa sababu, viwanja vilivyokamilika ni 8,316 kwa hiyo sio 845 kama alivyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia amezungumzia suala la kupunguza premium kwamba, pengine wananchi wanashindwa kuchangia. Naomba tukumbuke tu kwamba, premium hii awali ilikuwa ni 15% kwa viwanja vyote. Ikapungua ikawa 7.5%, lakini badaye Wizara ikapunguza zaidi kwenye zoezi la urasimishaji wanalipa 1% ya premium ambayo wanatakiwa kulipa tofauti na ule upangaji wa kawaida, ilitoka 7.5% wao wanalipa 2.5%. Kwa hiyo, kama ni suala la kupunguza ni kweli upunguzaji tumepunguza, lakini kwa sababu ni hoja inatolewa na Serikali ni sikivu basi tutaona namna kama kuna haja ya kupunguza tena au tuendelee na ileile 1%. Tukumbuke kodi hizi pia ndio zinarudi kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili amezungumzia kwamba, pesa ambazo zimekusanywa tulizotoa takwimu hapa ni tofauti. Si kweli anachosema, kwa mitaa mitano haiwezi kukusanya bilioni 15 kwa zoezi la urasimishaji, ukizingatia kwanza walipaji wenyewe ni wachache na nimetaja kati ya waombaji 147,000 tunaoshughulika nao sasa hivi ni 1,925 tu ambao wamekamilisha malipo yote. Kwa hiyo, si kweli kwamba, kuna pesa nyingi ambazo zipo,

Mheshimiwa Naibu Spika, kama pengine Mheshimiwa Mbunge anajua kuna mahali ambapo kuna pesa zimekusanywa na pengine hazijulikani zilipo, ameomba ukaguzi ufanyike, tutalifanyia kazi ili tuweze kujua ukweli wa Mheshimiwa Mbunge aliouleta na takwimu tulizonazo Wizarani ili tuweze kuwa na uhakika na alichokisema. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwanza naipongeza Serikali kwa majibu hayo na hasahasa kupima viwanja 56,792 katika kipindi kidogo cha miezi tisa, lakini Sikonge pale Mjini niao wananchi 2000 kwenye maeneo ya Ukanga wana viwanja 1400 na Majengo viwanja 6000 jumla viwanja 2000 kwa muda mrefu sana zaidi ya miaka 10 wanaomba hati hawajapatiwa.

Mheshimiwa Spika, sasa je, swali langu la kwanza wizara inawasaidieje wananchi wa Sikonge waweze kupata hati zao kwa haraka?

Mheshimiwa Spika, la pili je, Serikali haioni kwamba sasa hivi hapa nchini kuna uchumi mgumu kiasi ambacho wananchi wanapata shida kupata laki 150 kwenye miji ya vijiji kama Sikonge kupima kiwanja kimoja je, Serikali haioni kwamba hasa kuna wakati umefika wa kuwapa ruzuku ili waweze kupata hati zao za ardhi.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza anataka kujua tu kwamba ni lini utoaji hati utafanyika katika maeneo hayo. Tayari tulishafungua ofisi za mikoa na katika kasi ya utoaji hati sasa hivi inakwenda kwa kasi kubwa naomba nimuhakikishie tu kwamba ofisi yetu ya Tabora Mjini itakwenda kukamilisha hiyo na kwa kupitia majibu ninayotoa sasa basi wafike katika hayo maeneo mawili ndani ya Sikonge yenye viwanja 2000 ambao nasema kwamba hawajapewa hati mpaka leo, iwapo watakuwa wamekamilisha taratibu zote za umilikishaji.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anazungumzia suala la ruzuku kwamba 150,000 katika suala zima la upimaji ni gharama kubwa. Naomba niseme tu kwamba gharama hii si kubwa kama tunavyofikiri lakini pia inategemea na eneo husika maana kuna maeneo mengine mpaka sasa wanalipa 60,000 wanalipa 90,000. Wakiwa watoaji ni wachache unakuta kwamba ile gharama hata ya yule anayeenda kupima inakuwa kidogo ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuwa na watu wengi kwa wakati mmoja wanayohitaji gharama zile zinashuka kwa hiyo gharama zinashuka kutegemeana na volume ya kazi ambayo mpimaji anakwenda kufanya pale. Niwaombe wananchi kwamba suala la urasimishaji linakwenda kuisha 2023 kama nilivyosema kwenye jibu la msingi kwa sababu ilikuwa programu ya miaka kumi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, waongeze kasi sasa hivi ili kazi ile iishe halafu tuendelee na upimaji wa kawaida ambao hautakuwa na zoezi la urasilimishaji ambao majengo yale yamekaa kiholela na upimaji wake unakuwa kidogo ni mgumu ahsante.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika nashukuru, changamoto ambayo inakumba Sikonge ya ujenzi holela inakumba pia jiji la Dar es Salaam sasa tofauti na Sikonge Dar es Salaam tayari tuna Dar es Salaam City Master Plan ya 2012 mpaka 2032 ambayo tumeshaipitisha katika ngazi zote inasubiri tu utekelezaji. S nataka waziri uniambaie ni lini Serikali itaanza kutekeleza mkakati wa Dar es Salaam City Master Plan ili mji wetu upangike vizuri na uonekane na changamoto zote za mji kutokupangwa?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima Mdee Mbunge wa viti maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Dar es salaam tayari inayo master plan na ilishapitia katika nganzi zote lakini changamoto iliyopo pale katika utekelezaji wake bado katika halmashauri zinazohusika katika kufanya kazi ile kwa sababu ule utekelezaji unakwenda awamu kwa awamu kutegemeana na utaratibu wa mpangilio wa majenzi waliyoyaweka.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa sasa utekelezaji unaoendelea hawaruhusu pia hata katika ujenzi unaoendelea kuweza kujenga nyumba pengine katika maeneo ambayo master plan inazungumzia habari ya kwamba pana magorofa kadhaa, ukiomba kujenga nyumba ya kawaida unazuiliwa. Kama ni eneo la viwanda ukiomba kujenga nyumba ya kawaida unazuiliwa. Kwa hiyo, utekelezaji umeanza japokuwa space yake ni ndogo kutegemea jinsi mtu mji wenyewe wa Dar es Salaam ulivyokuwa umejengeka katika taratibu ambazo si ki mipango miji katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, lazima twende nao taratibu namna ya kuweza adapt kile ambacho tayari kimepangwa na wenye halmashauri zao ili kuweza kuhakikisha ile master plan inatekelezwa. Kwa hiyo, sisi kama wizara tutaendelea kushirikiana na TAMISEMI ili kuweza kuona ni jinsi gani ile master plan inatekelezwa bila kuleta athari kwa wananchi.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza, Halmashauri ya Geita Vijijini yenye makao makuu yake Nzela tumepima viwanja vikakamilika mwezi wa 12 mwaka jana na mwezi wa kwanza tulileta barua ya maombi kwa ajili ya kupitisha ile kamati ya ugawaji wa viwanja toka mwezi wa kwanza mpaka leo hatujawahi kupata majibu kutoka Ofisi ya Katibu Mkuu ambaye ndio mwenye idhini ya kuidhinisha hiyo kamati.

Je nini kauli ya Serikali kuhusiana na barua hiyo ya kuidhinisha hiyo kamati ilituendelee kuuza viwanja ambavyo viko tayari?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba nilichukuwe swali la Mheshimiwa Musukuma kama alivyosema kama kweli wameshaleta ofisini nikitoka hapa mchana nakwenda kuangalia kama yapo na tuweze kujua kwa nini mpaka leo haijaidhinishwa. Kwa sababu taratibu tunasema kamati zile zikishaletwa kazi ya waziri ni kuweza kuridhia ili zikaanze kufanya kazi. Sasa haiwezekana iwe imekuja kwa muda wote huo halafu majibu hajapa naomba nilichukuwe ili mchana niweze kuangalia nitampa majibu yake.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; kwa kuwa katika bonde lililoko katika Kijiji cha Nyenza kata ya Mabolilwa kumekuwa kuna mgogoro ambao umechukua miaka mitatu pale kwenye Mabaraza la Ardhi. Sasa kwa kuwa na wananchi wangu wameendelea kusumbuliwa kwenda na kurudi nilikuwa naomba kuuliza swali; je, sheria inampa mamlaka gani Waziri ya kuingilia kati endapo mgogoro umechukua muda mrefu kama huu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria Sura Namba 216 ambayo ndiyo inashughulika na utatuzi wa migogoro, Mheshimiwa Waziri hapaswi kuingilia maamuzi yanayotolewa na vyombo vya utoaji haki. Kama kuna changamoto yoyote ambayo inatokea katika maeneo hayo mlalamikaji anayo nafasi ya kumuona Msajili wa Mabaraza ya Ardhi kuweza kupeleka kero yake na atamsaidia hatua ya kwenda mbele zaidi.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba jina langu ni Francis Isack Mtinga, sio Mtenga, Mtenga ni Wachaga, Mtinga ni Wanyiramba.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa maelezo mazuri ya waziri ya kukiri mgogoro lakini nakiri sijaridhishwa kabisa na jibu walilolitoa. Na hivyo nitauliza swali moja tu la nyongeza ili nitoe na maelezo kidogo.

Mheshimiwa Spika, mpaka huu ni wa mkoa; mpaka kati ya Hanang’ na Mbulu na Wilaya ya Mkalama ni mpaka wa Mkoa wa Manyara na Mkoa wa Singida na amekiri kwamba tatizo hili ni la muda mrefu sana lakini majibu aliyoyatoa kwamba ni kupima, kupima hakutatui tatizo la mgogoro. Na tatizo hili limekuwa kubwa sasa kule Kijiji cha Eshkeshi, Wilaya ya Mbulu wameingia kilometa mbili katika Kijiji cha Ulamoto kule...

SPIKA: Uliza swali!

MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, naomba Waziri aniambie kwamba lini tutakwenda naye akafanye mkutano na wataalam kwa vijiji hivi ili kutambua mipaka ili kuondoa mgogoro huu na wananchi wafanye kazi za utawala vizuri, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Isaack.

Mheshimiwa Spika, suala la kutambua migogoro katika mpaka sio kufanya mikutano tu, kinachotakiwa pale ni kwenda na GN zinazohusika na kufanya tafsiri ya GN kuangalia zile coordinates katika yale maeneo. Naomba nimuhidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tukimaliza tutampa wapima watakwenda wakiwa na zile GN zinazotaja mipaka ya Wilaya zote mbili ili waweze kutambua na kuweza kubainisha mipaka. (Makofi)
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru kwa majibu ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa mradi huu unapita katika Kata za Kigogo, Mzimuni, Magomeni, na Hananasifu. Je, Serikali sasa iko tayari kutoa Tarehe au muda lini mapitio hayo yataenda kufanyika ili wananchi wa maeneo yale waweze kufahamu?

Swali langu la pili, ningependa kama ikiwezekana Serikali itoe tangazo mapema ili wananchi wale wote waweze kuwepo wakati tathmini hizo zikifanyika. Ahsante sana.
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Tarimba Abbas kwa maswali yake mawili.

Mheshimiwa Spika, naomba tu nimfahamishe kwamba katika mradi ambao unaendelea sasa pamoja na Kata alizozitaja mpaka sasa wananchi waliofikiwa ni 2,217 kati ya 2,432 ambao watafikiwa. Katika hao ambao wamefikiwa sasa katika ule mradi, asilimia 92 ni wananchi 2,057 wameshakubali wamefanyiwa uhakiki na kati yao ni 160 tu ambao hawajafikiwa. Kwa hiyo, kaya ambazo hazijafikiwa ni
215 na nadhani zipo katika yale maeneo ambayo umeyasema, hivyo wakifikiwa nadhani nao pia watapata huduma ile ile ambayo wamepatiwa wengine.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu kutoa tangazo, inawezekana likatoka, lakini huwezi ukalitoa kwa sasa kwa sababu procedure hiyo bado inaendelea. Kampuni iliyopewa kufanya kazi hiyo bado ipo uwandani inafanya kazi. Kwa hiyo, pale itakapokuwa imefikia kwenye hatua ambayo ni ya mwisho, kwa sababu maeneo yanayotwaliwa yote yanafahamika, basi wataambiwa wananchi, lakini kwa sasa huwezi kutoa tangazo kwa sababu bado pia tupo kwenye utaratibu wa kukamilisha.
MHE. NORA W. MZERU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu mkubwa wa kutenga maeneo ambayo hayana migogoro na ardhi ili kuwaruhusu wawekezaji waweze kuwekeza kwenye maeneo hayo?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI:
Mheshimiwa Spika, ahsante, nilitaka kujibu swali ambalo ameliuliza Mheshimiwa Mbunge kuhusiana na masuala ya utengaji maeneo ya uwekezaji. Maelekezo ya Serikali katika mikoa yote na katika halmashauri zote ni kuhakikisha kwamba wanatenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji na maeneo yale lazima yatambuliwe ili yaweze kuwa tayari kwa ajili ya uwekezaji na kama kuna suala pengine la wananchi katika maeneo yale wanatakiwa waongee nao na waweze kuyamiliki kama ni halmashauri yenyewe au ni Serikali ya Kijiji ili muwekezaji anapopatikana kusiwe na mgogoro.

Mheshimiwa Spika, pia tunayo yale maeneo ya EPZ ambayo yapo yalikuwa yametengwa nayo yamewekwa kwa ajili ya uwekezaji. Kwa hiyo kwa maana ya Serikali tayari tunalitambua hilo katika kuepusha migogoro na wananchi. Na niombe Mbunge anione kama kuna eneo maalum ambalo pengine linahitaji maelezo ya ziada.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa msingi wa maamuzi wa Mahakama unatokana na offer iliyotolewa tarehe 2 Julai, 1990 na offer hiyo ilikuwa ni ya miaka 33 mpaka leo tukihesabu ndugu Kambenga hana umiliki tena wa shamba hilo;

(a) Je, Serikali pamoja na nia njema ya mazungumzo yanayoendelea haioni sasa imefika wakati wa kurejesha shamba hilo kwa wananchi?

(b) Je, ni lini Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kuambatana na mimi kwenda kusikiliza wananchi hawa ili asikilize kilio chao? Ahsante.
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kunambi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la kuwa na offer ya miaka 33 na offer ikaisha haimnyimi uhalali kama ameomba tena kuendelea kulimiliki, na wakati huo huo kama hakuna mwombaji mwingine ambaye ameomba maana yake lile eneo linaweza likawa liko wazi kwa ajili ya wengine. Mpaka sasa tunavyoongea mwenye shamba hilo bado analitumia kwa hiyo tunaweza kusema kwamba bado anayo haki yake kwa ajili ya kumiliki eneo lile kwa sababu mpaka sasa hakuna mwombaji mwingine yeyote aliyeomba eneo lile.

Mheshimiwa Spika, suala la pili la lini niko tayari kuambatana naye, tutaangalia ratiba kwa sababu tayari tukimaliza Bunge hili tumeshajipangia ratiba ya kuzunguka katika Mikoa, tutaangalia Morogoro iko lini na tutafika kama iko kwenye awamu hii.