Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Gimbi Dotto Masaba (15 total)

MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Pamoja na Mkoa wa Simiyu kuzungukwa na Ziwa Victoria, bado una tatizo kubwa la upatikanaji wa maji safi na salama.
(a) Je, wakazi wa Bariadi, Maswa, Meatu, Itilima na Busenga watanufaika lini na uwepo wa maji ya Ziwa Victoria?
(b) Je, Serikali itaacha lini kutoa ahadi zisizotekelezeka kwa wananchi?
(c) Je, Serikali ya Awamu ya Tano inatoa ahadi gani katika kutekeleza mipango ya kuwapatia wananchi huduma ya maji?
NAIBU WAZIR WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba Mbunge wa Viti Maalum lenye vipengele (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaanza utekelezaji wa mradi wa maji safi kutoka Ziwa Victoria kwenda Mkoa wa Simiyu kwa Miji Mikuu ya Wilaya za Bariadi, Maswa, Meatu, Itilima na Busega na vijiji vilivyopo umbali wa kilomita 12 Kambi ya Mbomba Kuu.
Mheshimiwa Spika, mtaalamu mshauri aliwasilisha taarifa ya upembuzi yakinifu mwezi Oktoba, 2015 na hivi sasa anaendelea na usanifu wa mradi. Gharama za utekelezaji wa mradi mzima unakadiriwa kuwa kiasi cha shilingi za Kitanzania bilioni 747.8, sawa na Euro milioni 313.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kupitia Mashirika na wadau mbalimbali kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.
(b) Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitoa ahadi zinazotekelezeka, utekelezaji wa ahadi hizo huchelewa kutokana na upatikanaji wa rasilimali fedha kwa wakati.
Mheshimiwa Spika, katika jibu la msingi la (b) nitaomba uniruhusu kutoa maelezo ya ziada.
Mheshimiwa Spika, Serikali ya CCM kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi, baada ya kukamilisha Sera ya Maji ya mwaka 2002 ilianzisha programu ya kwanza ya utekelezaji wa miradi ya maji nchi nzima. Katika programu hiyo kulikuwa na miradi 1855. Miradi ambayo imekamilika hadi sasa ni miradi 1143, miradi inayoendelea ni miradi 454 na miradi ambayo inatarajiwa kuanza wakati wowote ni miradi 258.
Mheshimiwa Spika, lakini Mkoa wa Simiyu ni mkoa mpya na una matatizo ya maji na ni mkoa ambao unahesabika katika mikoa yenye ukame.
Kupitia programu hii kumekuwa na miradi ya Vijiji Kumi ambayo imetekelezwa katika Halmashauri zote za Wilaya, Wilaya ya Busega, Wilaya ya Itilima, Wilaya ya Meatu, Wilaya ya Maswa pamoja na Makao Makuu ya Mkoa wa Simiyu yaani Bariadi.
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea kutekeleza miradi ya maji ambayo lengo lake ni kufikisha huduma ya maji kwa asilimia 95 ya wakazi wa miji na asilimia 85 ya wakazi wa vijijini, ifikapo mwaka 2020. Miradi itakayotekelezwa ni pamoja na Mradi wa Maji Safi kutoka Ziwa Victoria kwenda Miji ya Igunga, Nzega, Tabora na Sikonge. Mradi wa Maji Safi Magu, Misungwi na Lamadi na Mradi wa Maji Safi Urambo kuelekea Kaliua.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Mkoa wa Shinyanga na Simiyu inaunganishwa kwa barabara ya vumbi, tofauti na mikoa mingine ambayo imeunganishwa kwa barabara za lami.
(a) Je, Serikali itaunganisha lini mikoa hiyo kwa barabara ya kiwango cha lami kwa kumalizia kilometa 102 zilizobaki katika barabara ya Lamadi - Mwigumbi kupitia Bariadi?
(b) Je, Serikali itaona umuhimu wa kuunganisha makao makuu ya Wilaya za Mkoa wa Simiyu kuunganishwa kwa barabara za kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbo Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mweshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Mwigumbi - Maswa - Bariadi - Lamadi yenye urefu wa kilometa 171.8 kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha ikiwa na lengo la kuunganisha Mikoa ya Simiyu, Shinyanga, Mara na Mwanza na kwa barabara ya lami. Sehemu ya barabara hii kuanzia Bariadi - Lamadi yenye urefu wa kliometa 71.8 tayari imejengwa kwa kiwango cha lami na imekamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2015/2016, TANROADS ilitia saini mkataba wa ujenzi na mkandarasi CHICO kutoka China kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami sehemu ya pili ya barabara hiyo kuanzia Mwigumbi - Maswa ambazo ni kilometa 50.3 kwa gharama ya shilingi bilioni 61.462. Hadi sasa mkandarasi yuko katika eneo la mradi na anaendelea na kazi za kujenga kambi, kuleta mitambo na wataalam kwa ajili ya kutelekeza mradi huo. Aidha, kwa sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kiwango cha lami wa sehemu ya Maswa - Bariadi ambazo ni kilometa 50.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kuwa kukamilika kwa barabara hii inayoendelea kujengwa kutawezesha Makao Makuu ya Wilaya za Busega, Bariadi na Maswa zilizoko katika Mkoa wa Simiyu kuunganishwa kwa barabara za lami. Wilaya nyingine zilizobaki zitaungwanishwa kwa barabara za lami kwa awamu kutegemeana na upatikanaji wa fedha.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Wakazi wengi wa Mkoa wa Simiyu huendesha maisha yao kwa kutegemea kilimo na ufugaji, ambapo Mkoa huo umepakana na maeneo makubwa na mazuri kwa kazi hizo jirani na Mbuga ya Serengeti:-
(a) Je, Serikali itatenga lini maeneo ya kilimo na mifugo kwenye vijiji vinavyopakana na Mbunga ya Serengeti?
(b) Je, Serikali itathamini lini mifugo na mazao ya wakulima hawa kama vile inavyothamini wanyamapori wa mbugani kwani huonekana ni halali kwa wanyama pori kuua/kuharibu mazao ya wananchi wakati siyo halali wananchi kuingiza mifugo au kuchimba hata mizizi ndani ya mbuga ya wanyama?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Matumizi Bora ya Ardhi na kwa kushirikiana na Halmashauri za Wilaya zenye vijiji vinavyopakana na mbuga ya Serengeti imeshachukua hatua za kuandaa mipango shirikishi ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji vinavyohusika. Tayari vijiji 73 katika Wilaya za Serengeti, Tarime, Bunda na Bariadi vimeshakamilisha mipango hiyo, kinachotakiwa sasa ni kwa Halmashauri hizo kuhakikisha kwamba vijiji ambavyo tayari vina mipango ya matumizi bora ya ardhi vinaitekeleza ipasavyo na kuimarisha usimamizi. Naomba Mheshimiwa Mbunge kushirikiana na Halmashauri husika ili vijiji visivyokuwa na mipango ya matumizi bora ya ardhi navyo viweze kuwa nayo ili faida za mipango hiyo ziwafikiwe wananchi wote.
Mheshimiwa Spika, Serikali inathamini mifugo na mazao ya wakulima na imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuepusha migogoro kati ya binadamu na wanyama pori na pia kuhakikisha kwamba maisha ya binadamu na mali zao yanalindwa kikamilifu. Hii inadhihirishwa na jinsi Serikali inavyosaidia vijiji kuwa na miradi ya ujirani mwema kwa vijiji vinavyozunguka maeneo ya hifadhi na vijiji hivyo kuwa na mipango shirikishi ya matumizi bora ya ardhi.
Aidha, kwa kutambua umuhimu wa maisha ya binadamu, mazao na mifugo Serikali imeweka utaratibu wa kuchukua hatua za haraka za kufukuza wanyama pori mara inapotokea wameingia katika makazi na mashamba ya wananchi na wakati mwingine inapobidi Serikali hutoa kifuta machozi au kifuta jasho kwa waathirika.
MHE.GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Kutokana na mpango wa Serikali kuhakikisha ifikapo mwaka 2025, Tanzania inafikisha uchumi wa kati.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha na kuhalalisha viwanda vya kutengeneza pombe aina ya gongo ili kuchochea uchumi wa nchi?
(b) Pombe hii aina ya gongo inapendwa kunywewa zaidi na watu wa vijijini. Je, Serikali haioni kwamba umefika wakati wa kuwaendeleza kielimu zaidi wataalam hao wanaotengeneza pombe hiyo ili wapate ujuzi kwa maslahi ya Taifa?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, viwanda anavyosema Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba ni tabaka la viwanda vidogo sana na viwanda vidogo. Viwanda hivi ni fursa ya sekta ya binafsi kuwekeza. Serikali inalenga viwanda vikubwa sana na miradi ya kimkakati.
Mheshimiwa Spika, kuhusu kuhalalisha pombe aina ya gongo kama ilivyo sasa ni jambo ambalo haliwezekani, ila sekta binafsi inashauriwa kuanzisha viwanda vitakavyotumia malighafi zinazotengeneza kinywaji hicho kwa lengo la kuzalisha kinywaji kinachokidhi viwango vya usalama na ubora wa chakula.
Naomba nirudie, kinywaji hicho kwa kuzingatia ubora na usalama wa mnywaji.
Mheshimiwa Spika, moja ya kigezo muhimu cha kuanzisha kiwanda ni uwepo wa soko. Kutokana na wananchi kupendelea kinywaji hiki, nitumie fursa hii kuwashauri wadau wa sekta hii kuwasiliana na ofisi za SIDO ambazo zinapatikana mikoa yote ili kupata mwongozo juu ya uanzishaji viwanda bora na salama vya aina hii.
Kwa upande wa Makampuni makubwa ya pombe nawashauri wachangamkie fursa hii kwa kutengeneza pombe yenye ladha ya gongo kwani baadhi ya wateja ni ile ladha inayowavutia na kupendelea kinywaji hicho.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Mkoa wa Simiyu ni miongoni mwa mikoa ambayo haina viwanda licha ya wananchi wake kuwa wakulima na wafugaji.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga viwanda vingi Mkoani Simiyu wikiwemo viwanda vya kusindika nyama, matunda, maziwa, ngozi, mafuta ya kula na nguo ili kuharakisha ukuaji wa uchumi na ongezeko la ajira kwa vijana?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, azma ya Serikali ya ujenzi wa uchumi wa viwanda imeainishwa vyema katika Mpango wa Pilli wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa mwaka 2016/2017 mpaka 2020/2021 wenye dhima ya kujenga uchumi wa viwanda ili kuleta mageuzi ya kiuchumi na maendeleo ya watu. Ili kufikia azma hiyo, ushiriki wa mchango wa mtu mmoja mmoja, makundi ya watu, taasisi za umma na taasisi binafsi unahitajika. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na wadau wengine tumeanza kutekeleza mikakati minne ya ngozi, mafuta ya kula, nguo na mazao jamii ya kunde. Wakati huo huo mapango wa wilaya moja, zao moja na uhamasishaji wa ujenzi wa viwanda chini ya SIDO unaendelea nchini kote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu na Watanzania kwa ujumla kuwa Mkoa wa Simiyu chini ya uongozi wa Komredi Anthony Mtaka umekuwa kinara wa kutekeleza mpango wa one district one product. Wilaya
tano za Bariadi, Busega, Itilima, Maswa na Meatu katika Mkoa wa Simiyu zimepangiwa kuzalisha mafuta ya alizeti. Vilevile Mkoa wa Simiyu una viwanda ambavyo vinaanzishwa kwa kuzingatia upatikanaji wa malighafi, teknolojia na soko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Maswa kimejengwa kiwanda cha chaki, Wilaya ya Bariadi na Itilima kitajengwa kiwandacha nyama na Wilaya ya Meatu kimejengwa kiwanda cha Maziwa. Hizi ni kazi ya mwaka mmoja na naweza kusema ni mwanzo mzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa taasisi, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) unakamilisha taratibu za kuwekeza kwenye kiwanda cha kuzalisha vifaa tiba vitokanavyo na pamba na bidhaa za maji (drip). Gharama za miradi hiyo inakadiriwa kufikia dola za kimarekani 36.5 na kutoa ajira za moja kwa moja 1,600 na zisizo kuwa moja kwa moja 5,000. Mradi huo unakadiriwa kutumia pamba tani 50,000 kwa mwaka. Aidha, Serikali ya Mkoa inaendelea na jitihada za kutenga maeneo ya uwekezaji kwa kuwalenga wajasiriamali wadogo, wa kati mpaka wakubwa bila kujali kwamba wanatoka ndani ya nchi au nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshauri Mheshimiwa Mbunge tushirikiane katika kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje kuanzisha viwanda na kusindika mazao ya kilimo katika Mkoa wa Simiyu ili kuhakikisha ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa vijana.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) katika Mkoa wa Simiyu na kukijengea uwezo wa kutengeneza vifaa vya baiskeli, pikipiki na magari?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia mradi unaofadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika kwa mkopo wa masharti nafuu imeendelea na maandalizi ya ujenzi wa chuo kipya cha mafunzo ya ufundi stadi cha Mkoa wa Simiyu ambapo kwa sasa Wizara imempata mtaalam wa kusanifu majengo na kusimamia ujenzi wa chuo hicho. Usanifu wa majengo hayo unatarajiwa kukamilika Novemba, 2017. Baada ya usanifu wa majengo hayo, zabuni ya ujenzi itatangazwa na ujenzi wa chuo hicho unatarajiwa kuanza Februari, 2018.
Mheshimiwa Spika, sambamba na kuanza kwa ujenzi wa chuo hicho, Serikali inaendelea kuandaa mahitaji halisi ya rasilimali watu, mitaala itakayotumika, mashine na mitambo, samani na vifaa vya kufundishia na kujifunzia. Maandalizi hayo ni kwa ajili ya kujengea chuo uwezo wa kutoa mafunzo ya ufundi stadi na kuwapata wahitimu wenye stadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutengeneza vifaa vya baiskeli, pikipiki na magari.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Zaidi ya 70% ya Watanzania, uchumi wao unategemea kilimo.
Je, kwa nini Serikali isifute ushuru wa matrekta kuanzia matano hadi kumi kwa kila kijiji nchini kwa ajili ya kilimo ili kuwawezesha wananchi kuondokana na kilimo cha mkono?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu cha 6(1) Sehemu ya Kwanza ya Jedwali la Sheria ya Kodi ya VAT ya mwaka 2014, kimebainisha misamaha ya kodi kwenye vifaa mbalimbali vya kilimo. Mojawapo ya vifaa vya kilimo vilivyosamehewa kodi ni matrekta, mashine za kuvunia (combine harvester), vifaa vya umwagiliaji, dawa za kuulia wadudu waharibifu wa mazao, vipuri vya matrekta na kadhalika. Hivyo basi, kwa mujibu wa jedwali hili, matrekta pamoja na vipuri vyake hayatozwi kodi na ushuru wa forodha.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Kampuni ya Group Sogesca Lanari Estero (GSLE) iliyokuwa inajenga barabara ya Nyanguge – Musoma kati ya mwaka 1979 – 1990 iliacha majengo katika Kijiji cha Yimtwila “A” ambapo Serikali kwa kushirikiana na wananchi wakaanzisha shule ya sekondari ya kutwa.
Je, ni kwa nini Serikali isitumie fursa ya uwepo wa majengo haya kupandisha hadhi shule hiyo kuwa ya kidato cha tano na sita kwa kuwa nyumba za walimu na mabweni yanaweza kupatikana?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, majengo yaliyokuwa kambi ya Kampuni ya Group Sogesca Lanari Estero iliyokuwa inajenga barabara ya Nyanguge kwenda Musoma kati ya mwaka 1979 hadi 1990 kwa sasa yanatumika kwa ajili ya Shule ya Sekondari ya Sogesca ambayo ni ya kutwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanikisha uwepo wa shule ya kidato cha tano na sita Wilayani Busega, Serikali imeweka kipaumbele cha kuanzisha shule ya sekondari Mkula kuwa ya kidato cha tano na sita katika mwaka wa fedha 2016/2017. Tayari Serikali imepeleka shilingi milioni 259 kwa ajili ya ujenzi wa bweni la wanafunzi, vyumba vya madarasa vinne, matundu ya vyoo kumi na ukarabati wa maabara. Mpango wa Serikali ni kuhakikisha shule za sekondari za kidato cha tano na sita zinaanzishwa katika kila tarafa.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Mkoa wa Simiyu hauna Mahakama ya Mkoa licha ya Mkoa huo kuanzishwa zaidi ya miaka mitano iliyopita. Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya ngazi ya Mkoa?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi katika mikoa yote Tanzania Bara. Mkoa wa Simiyu kama ilivyo mikoa mingine unayo Mahakama ya Hakimu Mkazi ambayo kwa sasa inatumia jengo la kupangisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ya Serikali ni kuwa na jengo la Mahakama kwa kila ngazi kwa kadiri itakavyowezekana. Tayari tunao mpango wa kujenga majengo katika kila ngazi ya Mahakama kwa awamu katika mwaka wa fedha 2017/2018. Simiyu ni moja ya mikoa mitano ambayo ujenzi wake wa Mahakama umeanza ambapo kwa sasa msingi umekamilika na hatua nyingine za ujenzi zinaendelea.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Wilaya ya Itilima haina Kituo cha Polisi cha Wilaya. Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Itilima?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi lina jumla ya Wilaya za Kipolisi 168 nchi nzima ambapo kati ya hizo, Wilaya 127 zina majengo kwa ajili ya Ofisi na Vituo vya Polisi vya Wilaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, uhaba wa vituo vya polisi pamoja na nyumba za kuishi askari nchini umesababishwa na kukosekana kwa rasilimali za kutosha kukidhi mahitaji ambayo ni makubwa. Hata hivyo, Serikali kupitia Jeshi la Polisi linafanya jitihada mbalimbali kama vile kutumia rasilimali zilizopo katika eneo husika pamoja na kushirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo ili kukabiliana na tatizo la uhaba wa vituo vya polisi nchini. (Makofi)
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI (K.n.y. MHE. GIMBI DOTTO MASABA) aliuliza:-
Tanzania inakabiliwa na tishio la mabadiliko ya tabianchi linalosababishwa na uchafuzi wa mazingira, hasa wa viwandani:-
Je, Serikali inatoa kauli gani kwa wamiliki wa viwanda wanaokiuka Sheria za Mazingira?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Doto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mhesimiwa Mwenyekiti, tatizo la mabadiliko ya tabianchi kwa kiwango kikubwa linasababishwa na uzalishaji wa gesi joto unaotokana na matumizi ya nishati kwa 47%, uzalishaji wa viwanda kwa 30% na usafirishaji 11% kwa shughuli za maendeleo katika nchi zinazoendelea kiviwanda hususan Ulaya, Marekani, Asia na Australia. Bara la Afrika kwa ujumla linachangia gesi joto kiasi kisichozidi 3%. Tanzania huzalisha kiasi cha tani 0.09 za hewa ukaa (Per Capital Emission) kwa mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, Tanzania inachangia kiasi kidogo sana katika tatizo la uzalishaji wa gesi joto ambazo ndiyo chanzo cha mabadiliko ya tabianchi. Hata hivyo, pamoja na kuchangia kidogo kiasi hicho Tanzania imeendelea kuathirika kutokana na athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi, kama vile kupungua kwa barafu ya Mlima Kilimanjaro, kuongezeka kwa usawa wa bahari, ukame, mafuriko ya mara kwa mara na mlipuko wa magonjwa. Tatizo kubwa linatokana na uchafuzi wa mazingira unaofanywa na baadhi ya viwanda nchini kwa kutiririsha majitaka yenye sumu na kemikali ambazo huathiri sana viumbe hai pamoja na mazingira kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania inayo Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya Mwaka 2004. Sheria hii imeweka misingi ya usimamizi, tathmini na kuchukua tahadhari kuhusu madhara kwa mazingira, yakiwemo ya viwandani. Kwa kuzingatia sheria hii, Serikali imekuwa ikielimisha na kuwatoza faini wamiliki wa viwanda wanaokiuka sheria hii. Aidha, wamiliki wanaoendelea kukaidi maelekezo na masharti wanayopewa hufungiwa kufanya shughuli na hupewa masharti kabla ya kuruhusiwa kuendelea na shughuli zao tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa wito kwa wamiliki wa viwanda kuzingatia utekelezaji wa sheria na mikakati mbalimbali iliyopo kwa ajili ya kuwezesha usimamizi endelevu wa hifadhi ya mazingira kwa faida yetu na vizazi vijavyo. Wamiliki wa viwanda wanatakiwa kuhakikisha Tathmini ya AAthari kwa Mazingira na Ukaguzi wa Mazingira (Environmental Audit) vinafanyika na kuzingatiwa. Aidha, wamiliki wa viwanda wanapaswa kutumia nishati rafiki kwa mazingira na kutumia teknolojia banifu katika uzalishaji wa bidhaa zao ili kusaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-

Serikali imekuwa ikiwapangia wakulima wa pamba bei ndogo wakati wa mavuno bila kuzingatia gharama kubwa walizotumia kipindi cha uzalishaji:-

Je, Serikali haioni sasa wakati umefika kuwaacha wakulima wauze pamba kwa bei kubwa wanayotaka wao?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kujibu maswali ya Waheshimiwa Wabunge, kwa ridhaa yako, naomba nitumie nafasi hii kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nguvu ya kuweza kusimama hapa.

Mheshimiwa Spika, pia nitumie nafasi hii kipekee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na wasaidizi wake kwa kuniamini na kuniteua katika hii nafasi ya Naibu Waziri wa Kilimo. Namuahidi Mheshimiwa Rais pamoja na wasaidizi wake, nitafanya kazi kwa uadilifu na kwa maarifa yangu yote katika kutekeleza majukumu ambayo wamenikabidhi.

Mheshimiwa Spika, pia nitumie nafasi hii kukushukuru wewe pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwa support yenu mpaka nikaweza kufika hapa. Ninawaahidi ushirikiano na naamini mtanipa ushirikiano katika kutimiza majukumu yangu. Pia nitumie nafasi hii kuwashukuru sana wapiga kura wangu wananchi wa Karagwe.

Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali haiwapangii wakulima bei ya kuuza pamba bali huratibu upatikanaji wa bei nzuri ya pamba kwa wakulima. Sheria ya Pamba Na.2 ya mwaka 2001 inaipa Serikali kupitia Bodi ya Pamba jukumu la kukaa na wawakilishi wa wakulima na kampuni za kununua pamba kukubaliana bei elekezi ambayo inazingatia gharama za uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, kwa wastani gharama za uzalishaji wa ekari ya pamba inakadiriwa kuwa Sh.488,000.

Ekari moja iliyotunzwa vizuri hutoa wastani wa kilo 1,000 sawa na kuzalisha kilo moja kwa Sh.488. Bei iliyopangwa na wadau wa pamba yaani bei elekezi ya msimu wa mwaka 2018/2019 ilikuwa Sh.1,100 ambapo kwa mkulima aliyezalisha kwa tija ya kilo 1,000 kwa ekari na kuuza kwa bei hiyo hakuuza chini ya gharama za uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, wakulima wa pamba ni wadau muhimu katika kupanga bei ya pamba kwa kila msimu. Serikali inatambua umuhimu huo, hivyo imefanya maboresho katika mfumo wa uuzaji kwa kufufua na kuimarisha vyama vya ushirika kwa lengo la kuongeza fursa ya wakulima kushiriki katika soko kupitia ushirika wao. Upangaji wa bei ya pamba huzingatia vigezo mbalimbali ikiwemo bei ya pamba nyuzi katika soko la dunia, kiwango cha kubadilishia fedha, bei ya mbegu za pamba, gharama za usafirishaji, uchambuaji na uwiano kati ya nyuzi na mbegu.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, katika mwezi Septemba, 2018, baadhi ya wakulima wa Mkoa wa Simiyu waliuza pamba kwa Sh.1,200 kwa kilo juu ya bei elekezi kutokana na mabadiliko ya bei ya pamba katika soko la dunia.

Mheshimiwa Spika, fursa ya wakulima wa pamba kuuza bei wanayotaka itaongezeka kwa kuwa Serikali inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika tasnia ya pamba hasa kuongeza viwanda vya kuchakata pamba hapa nchini. Aidha, Serikali inaendelea kujenga uwezo wa wakulima ili kuongeza tija katika zao la pamba na hatimaye kuongeza uzalishaji na pato la mkulima mmoja mmoja.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-

Serikali iliahidi kujenga Mradi mkubwa waMaji kutoka Ziwa Victoria kuanzia Nyashimo, Ngasamo, Dutwa, Bariadi, Itilima, Meatu na Maswa:-

Je, ni lini mradi huo utaanza na kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika,kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali itatekeleza mradi wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka katika Miji ya Nyashimo (Busega), Bariadi na Langangabilili, Maswa na Mwanhuzi. Mtaalam Mshauri anaendelea na kazi ya usanifu na uandaaji wa makabrasha ya zabuni na mradi huu utatekelezwa katika awamu mbili.

Mheshimiwa Spika, awamu ya kwanza itahusisha Miji ya Nyashimo (Busega), Bariadi na Lagangabilili pamoja na vijiji vipatavyo 170 vilivyo ndani ya kilomita 12 kutoka bomba kuu kila upande. Awamu hii itagharimu Euro milioni 105 ambapo kati ya hizo Serikali ya Ujerumani kupitia benki yake KfW itatoa Euro milioni 25naGreen Climate Fund(GCF) Euro milioni 80. Ujenzi waawamu ya kwanza unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2019 na kukamilika mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, awamu ya pili ya mradi itahusisha Miji ya Mwanhuzi, Maswa na vijiji vipatavyo 83. Kwa sasa Serikali inaendelea na majadiliano na Green Climate Fund ili kupata fedha kiasi cha Euro milioni 208 zitakazotumika kugharimia utekelezaji wa awamu hii. Ujenzi wa awamu ya pili utaanza baada ya kukamilisha taratibu za upatikanaji wa fedha hizo. Kukamilika kwaawamu zote kutawanufaisha wananchi wapatao 834,204.
MHE. ANATHROPIA L. THEONEST (K.n.y. MHE. GIMBI D. MASABA) Aliuliza:

Wilaya mpya ya Itilima haina Mahakama ya Wilaya, jambo linalosababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi kwenda Wilaya jirani ya Bariadi kupata huduma hiyo:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya Itilima?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Wilaya ya Itilima kwa sasa haina Mahakama ya Wilaya na wananchi wanalazimika kusafiri umbali mrefu takriban kilometa 37 kufuata huduma katika Wilaya ya Bariadi. Aidha, changamoto hii ipo kwenye Wilaya 27 nchini, ambazo zinapata huduma katika wilaya za jirani. Hii inatokana na ukweli kwamba Mahakama ya Tanzania bado inakabiliwa na uhaba wa majengo katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimekuwa nikieleza katika Bunge lako, Mahakama imejiwekea mkakati wa kutatua changamoto hii hatua kwa hatua kupitia mpango wake wa miaka mitano na kujenga na kukarabati majengo ya Mahakama kwa ngazi zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ya Wilaya ya Itilima ipo kwenye mpango wa kujengwa kwa mwaka 2019/ 2020 pamoja na Mahakama nyingine za Wilaya za Busega, Kyerwa, Misenyi, Gairo, Mbogwe, Songwe, Rufiji, Kibiti, Nyang’hwale, Mvomero, Uyui, Kaliua, Uvinza, Buhigwe, Kakonko, Chamwino, Chemba, Ikungi, Mkalama, Butiama, Rorya, Ubungo, Malinyi, Tanganyika, Mkinga, Kilosa, Kilombero, Hanang na Nkasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima kwa kutupatia kiwanja cha kujenga Mahakama ya Wilaya yenye ukubwa wa mita za mraba 5,028. Aidha, nitoe pia shukrani zangu za dhati kwa Halmashauri za Wilaya zote nilizozitaja kwa kutupatia viwanja kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya Mahakama. Ahsante.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-

Wananchi wa Wilaya ya Itilima, Mkoani Simiyu huvamiwa na kuharibiwu mazao yao na wanyama aina ya tembo na Serikali hutoa fidia kidogo na wakati mwingine kutowafidia kabisa:-

Je, Serikali inatoa ahadi gani kwa wakulima juu ya fidia kwa waathirika wa uvamizi huo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vinavyoathiriwa na uvamizi wa wanyamapori hasa tembo katika Wilaya ya Itilima ni vile vinavyopatikana na Pori la Akiba Maswa. Kutokana na changamoto hiyo, Wizara huchukua hatua kadhaa ili kunusuru maisha na mali za wananchi. Hatua hizo ni pamoja na kushughulikia matukio ya uvamizi wa tembo kwa haraka iwezekanavyo pindi yanapojitokeza. Aidha, Wizara imeendelea kutoa elimu ya uhifadhi kwa wananchi kuhusu namna ya kujilinda na kuepuka kulima kwenye shoroba na mapito ya wanyamapori.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imekuwa ikitoa kiasi fulani cha fedha kwa wananchi wanaoathirika na matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu ikiwa ni kifuta jasho na kifuta machozi na siyo fidia kwa mujibu wa Kanuni za mwaka 2011. Mfano, katika kipindi cha miaka miwili ya 2016/2017 na 2017/2018 jumla ya Sh.35,614,000 zimelipwa kwa wananchi 336 wa Wilaya ya Itilima.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kwa sasa Wizara imepokea maombi ya malipo ya kifuta jasho na kifuta machozi ya wananchi 238 kutoka katika vijiji 7 vya Nyantungutu, Ndingho, Ngwalali, Pijulu, Mbogo, Mwamtani B, Lungwa na Longalombogo. Wizara inaendelea kuhakiki maombi hayo na itawalipa wananchi baada ya kujiridhisha na hatua za uharibifu na kiwango cha kifuta machozi wanachostahili kulipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kiasi kinacholipwa ni kidogo na Serikali inatambua suala hili ambapo kwa sasa Wizara inafanya mapitio ya sheria na kanuni za uhifadhi wa wanyamapori, moja ya masuala yanayozingatiwa katika mapitio hayo ni suala la kifuta jasho na kifuta machozi.