Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Kunti Yusuph Majala (3 total)

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunapoingia kwenye chaguzi vyama pamoja na wagombea huwa wanawaahidi wananchi ili waweze kuwaamini na kuweza kuwapa nafasi katika nafasi mbalimbali wanazogombea. Mnamo tarehe 5 Oktoba, 2015 mgombea Urais kupitia Chama cha Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akihutubia katika uwanja wa Barafu Manispaa ya Dodoma alikutana na mabango mbalimbali ya wananchi wa Manispaa ya Dodoma wakilalamikia suala la CDA na mgombea Urais Mheshimiwa John Pombe Magufuli aliwaahidi wakazi wa Manispaa ya Dodoma endapo watampatia kura za kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jukumu lake la kwanza ni kuifuta CDA.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, wakazi wa Manispaa ya Dodoma wanapenda kujua ni lini ahadi hii ya Mheshimiwa Rais itakwenda kutekelezwa? Ahsante
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika naomba kujibu swali la Mhesimiwa Kunti, Mbunge wa Dodoma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa anafanya ziara maeneo mbalimbali amekuwa akitoa ahadi kadhaa. Nataka nirudie kusema tena kwa Watanzania kwamba ahadi ambazo Mheshimiwa Rais ameziahidi tutajitahidi kuzitekeleza kwa kiasi kikubwa ikiwemo na uboreshaji wa Mji wa Dodoma, pia moja ya ahadi yake ilikuwa ni kwamba katika awamu yake hii kufikia mwaka 2020 atahakikisha Serikali inahamishia Makao yake Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ikiwa ni moja kati ya mambo ambayo aliyaahidi na tumeyatekeleza, mbili kwa kuwa tayari Serikali imehamia Dodoma lazima sasa tuandae utaratibu wa uboreshaji wa mazingira ya Mji wa Dodoma ili utawala wake, uendeshaji uweze kuwa rahisi ikiwemo na kupitia sheria mbalimbali zilizoiunda CDA, kuzifanyia mapitio na kuziboresha ili tuweze kuachana na CDA tuwe na mfumo ambao utatoa nafasi kubwa ya kukaribisha watu wa kawaida, wawekezaji na kuitumia ardhi iliyopo kwenye Manispaa katika kuwekeza au vinginevyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa nikiri kwamba kwa Sheria ya CDA huwezi kuleta mwekezaji hapa kwa sababu ni CDA pekee ndiyo imepewa ardhi hii na wao ndiyo waliopewa hati na ardhi Makao Makuu. Kwa hiyo wao wasingeweza kutoa hati kwa wananchi wanaojenga au wanaowekeza hapa, ili kuwapa nafasi wananchi kuwa na hati ya umiliki wa ardhi lazima tufute Mamlaka ya CDA ili tuweze kutumia Sheria ya Ardhi katika kutoa ardhi iliyopo hapa ili tuweze kukaribisha wawekezaji na uboreshaji wa mpango ambao sasa tumeukamilisha kuhamia Makao Makuu Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nikutoe wasiwasi kwamba sasa tunafanya mapitio na Mheshmiwa Rais ameshatoa maagizo Tume imeshaundwa inafanya mapitio ya namna bora ya kuifuta CDA lakini kupitia sheria zilizoiweka CDA, hiyo ndiyo hatua ambayo tumeifikia na katika kipindi kifupi tutakuwa tumeshatoa taarifa. Ahsante.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipatia na mimi nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, tangu nchi yetu imepata uhuru, Watanzania zaidi ya asilimia 75 ni wakulima kutokana na Serikali kutangaza kilimo ni uti wa mgongo lakini wakulima wetu hawa ambao ni Watanzania wameendelea kulima kilimo cha kutegemea mvua ya Mwenyezi Mungu ambacho kimekuwa hakina tija kwao wala tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nini mkakati wa Serikali wa kuwatoa Watanzania wakulima kwenye kilimo hiki kisichokuwa na tija kwao na kwa Taifa letu kuwapeleka kwenye kilimo ambacho kitaweza kutuondoa Watanzania kwenye wimbi la umaskini na kwenda kufikia sasa kwenye uchumi wa kati ambao utakaokwenda kukidhi mahitaji ya muonekano kwa Watanzania wetu? Nakushukuru.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunty Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba Serikali yetu sasa hivi inasisitiza kilimo ili kiweze kutoa manufaa au tija kwa wale wanaolima na wito huu wa kulima mazao haya ya biashara na chakula ni mkakati ule ule wa kuongeza tija kwa kilimo chetu. Ni kweli kwamba tukitegemea kilimo kinachotegemea hali ya hewa kama mvua pekee hatuwezi kupata tija. Nini tumekifanya Serikali.

Mheshimiwa Spika, Serikali ina taasisi au Kurugenzi ya Umwagiliaji ambayo yenyewe tumeipa bajeti ya kuhakikisha kwamba wanahakikisha tunafufua kilimo cha umwagiliaji nchini kitakachomwezesha mkulima kulima wakati wote masika, lakini wakati wa kiangazi ili uzalishaji uwe mkubwa na mkulima anapolima apate mazao ya kutosha, akiamua kuyauza kama atapata ziada, atapata uchumi lakini pia kumhakikishia usalama wa chakula pale anapozalisha, lakini kama ni zao tu la biashara kuendelea kumtafutia masoko. Kwa hiyo, mkakati wa Serikali katika hili ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na kilimo cha aina zote mbili cha kutegemea hali ya hewa ya mvua lakini pia na umwagiliaji ambao pia tumeimarisha na tunaendelea pia kubaini maeneo yanayofaa kwa umwagiliaji na kuanzisha miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano, Mheshimiwa Kunti yeye anatoka Chemba, Chemba ni eneo ambalo limepitiwa na mto mkubwa sana ambao unatiririsha maji mpaka maeneo ya Bahi. Mto ule unapitisha maji masika pamoja na kiangazi. Mkakati ambao tunao maeneo yote yanayopita maji yale kwenye mto pembezoni tunaona wakulima wapo ambao wanalima. Sasa tunawaanzishia miradi ya umwagiliaji ili wakulima hao waweze kulima kilimo ambacho kitawapatia fursa ya kutosha ili waweze kunufaika na kilimo hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, malengo yetu kilimo chetu nchini kiwe na tija kwa wakulima, kituletee mazao ya chakula ya kutosha, pale ambapo wanalima mazao ya kibiashara basi wapate mazao ya kibiashara ya kutosha. Kwa ujumla wake tutaanza kuleta tija kwa wakulima, lakini pia kwa nchi na kuifanya nchi yetu kuwa na usalama wa chakula cha kutosha kwa kulima chakula cha kutosha na ziada. Huo ndiyo mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba Serikali na wananchi wake wanalima kilimo hiki. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipatia nafasi ili niweze kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Spika, kupitia sera ya Serikali kupitia Wizara ya Habari na Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kutoka kwenye mfumo wa analogia kwenda kwenye mfumo wa kidigitali, kwa kutekeleza sera hiyo Serikali imeamua kwa kuanza kwenye mfumo wa malipo kutaka wananchi kuanza kulipa kwa njia ya kielektroniki lakini mfumo huu umekuwa na changamoto kubwa sana ya makato makubwa lakini pia na mawasiliano pia mtandao kutokuwa sawa. Sasa swali langu;

Je, ni nini mkakati wa Serikali moja kupunguza makato lakini pili kuhakikisha inaboresha mfumo wake ili mfumo uweze kufanya kazi kwa uthabiti ili kuondokana na kadhia kubwa ambayo Watanzania wanaipata kwa namna ambavyo jinsi mtandao huu unavyofanya kazi?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Mbunge Mkoa wa Dodoma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uko ukweli kwamba Tanzania kutokana na maendeleo ya tehema na sisi tumeanza kutekeleza mifumo mbalimbali kwa ajili ya kurahisisha utendaji kazi ndani ya Serikali, ikiwemo na ukusanyaji wa mapato kwa mfumo wa kielektroniki.

Mheshimiwa Spika, Tananzia ni moja kati ya nchi ambazo zinaanza siku za hivi karibuni kutekeleza mifumo mbalimbali kielektroniki. Tunapitia katika nyakati kadhaa za mafanikio lakini pia changamoto tunapoelekea kujiimarisha. Ukusanyaji wa mapato yetu kielektroniki ni mfumo ambao unaendelea vizuri sasa pamoja na hizo changamoto. Sasa, ili kukabiliana na changamoto hizi yako maelekezo thabiti yaliyofikiwa na serikali yetu kupitia Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, moja ameanzisha Wizara maalumu inayoshughulikia Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa lengo la kufanya mapitio ya kina kwenye mifumo hii na kuimarisha tehama hapa nchini, na kusimamia kampuni zote za taasisi na sekta binafsi ambazo zinajishughulisha na mawasiliano ili kuimarisha mifumo hii ya mawasiliano. Kwa hiyo kuna tozo kuwa kubwa lakini pia kuna mtandao kutofanya kazi vizuri suala la tozo hili ni wale walioamua tozo hiyo kuwepo. Haya tunayafanyia kazi, na tumewasikia Waheshimiwa Wabunge mara kadhaa na wananchi pia kuitaka Serikali ipitie makato mbalimbali au tozo mbalimbali ambazo zinazotozwa kwenye maeneo mbalimbali, hilo linafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, suala la mtandano hili Mheshimiwa Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari atakuja mbele yetu Waheshimiwa Wabunge kuja kuwasilisha mpango
wa bajeti, mpango wa kazi ambao tutaufanya mwaka ujao na kuomba ridhaa ya fedha. Moja kati ya mambo ambayo nitamwagiza hapa ni kuja kueleza nini wizara inafanya katika kuimarisha mifumo ya mawasiliano na hasa hii mitandao kuwa imara bila kukatika. Kwa sababu hata pia upande wa Serikali tunapata hasara sana lakini baadhi ya watu ambao wanapata vitendea kazi vya kielektroniki kwa kuzima na kusingizia kwamba mtandao haupo na kujipatia mapato, pia Serikali tunapata hasara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunataka tuimarishe eneo hili ili tuwe na mfumo mzuri wa mtandao kupitia taasisi zetu zinazofanya kazi ya kusambaza mitandao lakini pia Serikali inaimarisha tozo mbalimbali ili kuleta unafuu kwa Watanzani.

Mheshimiwa Spika, malengo yetu tunapokwenda kwenya maendeleo ya tehama tuwe na tehama ambayo inaweza kumhakikishia mtanzania kuitumia katika shughuli zake binafsi na hiyo ndio mwelekeo wetu.

Mheshimiwa Spika, hayo ndio maelezo ya eneo hili ahsante sana. (Makofi)