Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Lathifah Hassan Chande (8 total)

MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, mpango huu wa REA upo kwa ajili pia ya Mkoa wa Lindi hadi Lindi Vijijini, lakini mpaka sasa hivi maeneo mengi ya Mkoa wa Lindi bado hayana umeme. Je, ni vijiji vingapi katika Mkoa wa Lindi ambavyo vinatarajia kupewa umeme wa REA katika bajeti ya mwaka 2016/2017?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vinavyotarajiwa kuunganishwa umeme katika Mkoa wa Lindi kupitia REA Awamu ya III ni 117. Ahsante sana.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kutokana na kwamba Serikali inanunua ndege na kuikodisha ATCL, hata hivyo umiliki huu wa ndege uko kwa Wakala wa Ndege za Serikali. Kwa maana hiyo basi, ATCL inakodisha hizi ndege. Sasa je, ATCL inatoa malipo yoyote kwa Serikali kwa ajili ya kukodisha ndege hizi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kwamba mpaka sasa hivi Serikali inaisimamia management pamoja na Bodi ya ATCL, kwa maana hiyo ATCL haina mamlaka huru ya kutekeleza shughuli zake za utawala. Sasa swali langu ni kwamba, Serikali ina mpango gani wa kuiachia management na Bodi ya ATCL ili iweze kufanya mamlaka yake kwa uhuru na kuweza kufanya shughuli za kibiashara kwa ajili ya kuipatia Serikali mapato ambayo itakuwa ni faida endelevu? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna malipo yanayolipwa na ATCL kwa mmiliki wa ndege, lakini nadhani Mheshimiwa Lathifah anafahamu, mmiliki wa ndege, TDFA, inamilikiwa kwa asilimia 100 na Serikali na kwa upande mwingine mwendesha ndege au mkodishaji wa ndege hizo ni ATCL ambaye naye anamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100. Hiyo haifanyi ATCL apunguze nguvu katika kuhakikisha kwamba anafuata shughuli za biashara na hatimaye analipa gharama za kukodisha ndege hizo. Kwa hiyo, zinalipwa na takwimu tu bahati mbaya sina, ukizitaka nitakuletea uone hadi sasa ATCL wameshalipa kiasi gani kwa TDFA ambao ndege zao wamezikodisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uhuru wa bodi na management, nimhakikishie Mheshimiwa Lathifah, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ni moja kati ya Wizara zinazohakikisha taasisi zake zinazofanya shughuli za kibiashara zinafanya shughuli kibiashara na haziingiliwi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi hizo zikiwa ni pamoja ATCL, haiingiliwi, bodi ina mamlaka kamili ingawa tu wanalalamika kuna vikao vingi sana vya taasisi za Kiserikali na taasisi za Bunge, lakini hizi zote ni kwa mujibu wa sheria. Sheria za Bunge zinawataka wao wawajibike Bungeni kila wanapotakiwa kuwajibika na Sheria za Msajili wa Hazina zinawataka wao wawajibike kwa Msajili wa Hazina kila wanapoona kwamba wanahitaji kuwajibika, lakini huko siyo kuingilia uhuru wao. Taasisi hizi zinatekeleza wajibu wao kwao, wao wanaendelea kuwa huru katika kufanya maamuzi yao.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kutokana na kwamba demand ya Soko la Dunia ni ufuta mweupe, lakini Tanzania tumekuwa tukilima ufuta wa brown ambao bei yake inakuwa haina thamani kubwa kama ilivyo ufuta mweupe: Je, Serikali ina mpango gani wa kuweza kuwasaidia wakulima wa ufuta nao waweze kuanza kulima ufuta mweupe ili kuweza kuongeza kipato? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, ni juu ya Kiwanda cha Korosho kilichopo Lindi, Kiwanda cha TANITA ambacho kilikuwa kinaendeshwa na Serikali na kiliweza kuwapatia ajira wananchi wengi. Sasa hiki Kiwanda cha Korosho, TANITA, kimebinafsishwa ambapo hamna shughuli yoyote inayoendelea baada ya ubinafsishwaji huu na kupelekea wananchi kukosa ajira. Je, Serikali ina mpango gani juu ya kukifufua kiwanda hiki kutokana na kwamba Sera ya Serikali ya Awamu ya Tano ni Tanzania ya viwanda? Ina mpango gani juu ya kufufua hiki kiwanda na viwanda vingine vingi vilivyoko Mkoani Lindi? Ahsante.
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lathifah ameuliza swali lake la kwanza wakati muafaka; bajeti ya Wizara ya Kilimo inafuata nami nitamhimiza Waziri wa Kilimo kwamba tulete mbegu zinazozalisha ufuta mweupe ambao una soko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kiwanda cha korosho, Serikali ina mpango gani? Mpango wetu ni kuhakikisha kwamba viwanda vyote vilivyobinafsishwa vinafanya kazi. Hatuendi kwa kasi inayotakiwa kama nitakavyoeleza kwenye bajeti yangu kesho kutwa, ni kwa sababu viwanda vingine vina matatizo ya mikataba ya kisheria, lakini dhamira yetu ni hiyo na tutahakikisha viwanda vyote vinafanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na viwanda hivi, wako wawekezaji wanakuja na nitahakikisha Mheshimiwa Mbunge tunashirikiana kwamba Waheshimiwa Wabunge wanaokuja waende Lindi na nimeshazungumza hata na ndugu yangu, viwanda vingi vitakwenda vitaanzishwa ikiwemo na kufufua vile vya zamani.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Serikali ilisema kwamba itagawa sulphur bure na matokeo yake sulphur iliyogaiwa, nyingi ilikuwa ni feki na nyingine ilikuwa imeshapitwa na muda, yaani ime-expire. Hii inaweza kupelekea kuharibu zao hili la Korosho. Sasa Je, Serikali ikiwa kama mdhibiti, ilikuwa wapi mpaka hii sulphur ikaweza kuingia nchini na hadi kumfikia mkulima?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili ni kwamba, sasa hivi Mkoa wa Lindi wamelima kwa wingi zao la choroko na mbaazi ambalo wamekosa soko hadi kupelekea gunia moja la kilo 100 kuuzwa kwa Sh.15,000/=.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapo miaka ya nyuma, Bunge hili lilipitisha Sheria ya Exchange Commodity ambapo ilikuwa na mpango wa kuanzisha Exchange Commodity Market na mpaka dakika hii tayari Ofisi kwa ajili ya Exchange Commodity Market imepatikana na hadi savers zimekuwa set up lakini hakuna operation zozote zinazoendelea; kitu ambacho soko hili la Exchange Commodity lingeweza kuwasaidia wakulima waweze kupata soko la uhakika kwa ajili ya mazao mbalimbali. Sasa je, Serikali ina mpango wa kuanza lini operations katika Commodity Exchange Market? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na viuatilifu au sulphur feki au iliyopitwa na wakati, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba hakuna sulphur feki wala iliyopitwa na wakati ambayo imesambazwa kwa wakulima. Naomba yeyote mwenye ushahidi wa mkulima mmoja tu ambaye ameuziwa au amepewa sulphur feki au ambayo imepitwa na wakati anipe ushahidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nawahakikishia kwamba hakuna sulphur feki wala ambayo imepitwa na wakati ambayo imesambazwa kwa wakulima. Kilichotokea katika taarifa zile mlizoona kwenye vyombo vya habari ni kwamba kulikuwa na sulphur ambayo iko kwenye maghala ambayo imepitwa na muda, ime-expire lakini haikuwa kwa ajili ya kugawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la commodity exchange, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba utaratibu wa commodity exchange hautafuti soko, yaani siyo kwamba ukishatumia commodity exchange basi unakuwa na uhakika wa soko. Kama soko halipo ni kwamba halipo tu. Commodity exchange haina tofauti kimsingi na utaratibu wa sasa tunaotumia wa stakabadhi ghalani. Tofauti yake kidogo tu ni kwamba yenyewe inatumia teknolojia zaidi, lakini kama hakuna mnunuzi hutapata kwa kutumia commodity exchange.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, nimhakikishie kwamba Serikali kwa sasa imejiwekeza zaidi katika kuimarisha utaratibu tulionao wa stakabadhi ghalani kwa sababu ili tuweze kufikia kwenye commodity exchange tunahitaji vitu vingi. Tunahitaji kuwa na maghala ambayo ni ya kisasa zaidi, tunahitaji teknolojia, tunahitaji kuweza kuzalisha kwa utaratibu unaotakiwa na masoko ya nje lakini vilevile tunahitaji wakulima wetu waweze kuzalisha kwa viwango vile ambavyo vinahitajika. Kwa hiyo, kwa sasa jitihada ya Serikali siyo kwenye commodity exchange, tutaelekea kule, lakini kwa sasa tunaweka nguvu nyingi kwenye utaratibu wa stakabadhi ghalani.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta soko kwa ajili ya mazao ya mikunde. Changamoto iliyotokea ni kwamba India ambayo ndiyo nchi inayonunua mazao ya mikunde, kwa mwaka huu wana ziada ya asilimia 30 na ndiyo maana mbaazi zetu, dengu zetu na choroko zimepata changamoto. Hata hivyo kwa kupitia Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kununua mbaazi za wakulima, lakini huko mbele ya safari tunagemea tuanze kuuza zao hilo la mbaazi kwa utaratibu wa stakabadhi ghalani tukiamini kwamba kuuza kwa pamoja kutasaidia bei iwe nzuri zaidi. (Makofi)
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Serikali imesema kwamba itaunda timu maalum kwa ajili ya kushughulikia suala hili la Mtawango, lakini Kamati ya LAAC ilituletea taarifa yake hapa Bungeni ambayo ilionesha kwamba kuna ufisadi mkubwa unaoendelea katika miradi mbalimbali ya maji hapa nchini. (Makofi)
Je, Serikali ipo tayari kuunda Tume ya Kitaifa itakayoweza kuchunguza miradi mbalimbali ya maji hapa nchini na kutuletea taarifa ya ripoti yake hapa Bungeni kama ambavyo Kamati ya LAAC ilipendekeza?
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Ng’apa wa maji safi na salama ambao uko Lindi uliopelekea hadi Rais akamtumbua na kumfukuza nchini yule mhindi mpaka leo hii haujakamilika na kusababisha wananchi wa Lindi kukosa maji salama na safi.
Je, ni kwa nini mradi huu mpaka leo hii haujakamilika pamoja na kuwepo na maagizo ya Rais? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni maelekezo ya Kamati ya LAAC ambayo yaliweka maazimio ya kuunda mpaka Tume kuhusu kuchunguza miradi ya maji, kwa sababu tayari maazimio hayo yalikubalika na Bunge nafikiri hebu tuyaache sasa, hayo maazimio yaweze kufanyiwa kazi badala ya kuunda tume nyingine ya pili.
Swali la pili, ameulizia kuhusu Mradi wa Ng’apa nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi wa Ng’apa umekamilika na sasa hivi unatoa maji Mjini Lindi, kama una ndugu zako wako Lindi kule naomba uwapigie simu, tayari mradi umekamilika na nimetoa tena fedha shilingi milioni 500 ili tuweze kuweka miundombinu ya kusambaza maji Mjini Lindi ili maeneo mengi yaweze kufaidika na mradi wa Ng’apa.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa Mikoa ya Lindi, Mtwara na Pwani ina mito mingine mikubwa kama Mto Mbwemkuru, Mto Matandu na Mto Lukuledi lakini cha kushangaza maeneo yanayozungukwa na hiyo mito bado yanakabiliwa na tatizo kubwa la uhaba wa maji.
Je, Serikali ina mpango gani wa kutumia mito hiyo katika kujaribu kutatua tatizo hili la uhaba wa maji? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa kuwa hii mito mikubwa kama Mto Rufiji na Mto Ruvuma na mingineyo iliyopo katika Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma ni mikubwa ambayo ingeweza hata kusaidia katika upatikanaji wa umeme.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwezesha mito hii kuwekwa kwenye mpango wa hydro-electric kwa ajili ya kuleta umeme katika vijiji ambavyo REA imeshindwa kuvifikia? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza amehoji, ni kweli tunayo Mito ya Mbwemkuru, Matandu, Lukuledi katika eneo hilo, lakini sasa mito hiyo Mheshimiwa Mbunge na mimi nimekaa kidogo kule, uzoefu unaonesha kwamba inakuwa na maji mengi sana kipindi cha masika lakini baadhi ya mito kipindi cha kiangazi inakauka. Kwenye taratibu tunazoendelea nazo kufanya utafiti ili tuweze kujenga mabwawa makubwa ya kuvuna maji basi tutahakikisha kwamba mabwawa hayo tutayawekea na skimu za umwagiliaji ili wananchi wanaoishi pembezoni na hiyo mito waweze kufaidika na kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, umeuliza kuhusu umeme. Mheshimiwa Mbunge, zipo taratibu zinaendelea kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunaweka kituo cha kuzalisha umeme katika Mto Rufiji kwenye hilo neno linaitwa Stiegler’s Gorge ambapo kutakuwa na kilimo kikubwa pamoja na kuzalisha umeme mkubwa ili tuweze kuongeza nguvu ya umeme katika Tanzania.
Kwa hiyo, Serikali yako Mheshimiwa Mbunge ya Chama cha Mapinduzi tayari imeshaliona hilo na inaendelea kufanya mawasiliano na wafadhili mbalimbali pamoja na kutumia vyanzo vya ndani ili tuweze kutekeleza huo mradi. (Makofi)
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, masharti ya mauzo hayo yaliruhusu ukodishwaji?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kutokana na kwamba malengo ya Serikali ilikuwa ni kuweza kubangua tani 200,000 za korosho na hii ikapelekea kwamba hata Bodi ya Korosho pamoja na mfuko wa kuendeleza zao hili la korosho ulitenga pesa kwa ajili ya kujenga viwanda katika Mkoa wa Pwani, Ruvuma pamoja na Mtwara. Sasa wakati tunasubiria hivyo viwanda viweze kujengwa kwa nini Serikali isifufue viwanda vilivyoko ili kuweza kutimiza hayo malengo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, kimsingi Serikali ina taarifa juu ya huo ukodishaji kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi.
Katika swali lake la pili nipende tu kuzidi kumuhakikishia ni kwamba kama amekuwa akifuatilia hata kupitia bajeti yetu, lakini pia ziara mbalimbali tunazofanya, Serikali imeamua kuona kwamba viwanda vyote vilivyobinafsishwa vinafanya kazi yake kama iliyokusudiwa, lakini pia kuhamasisha viwanda vingine viweze kufanya kazi hiyo ikizingatiwa kwamba korosho ni zao kubwa na ni zao ambalo linapendwa duniani na hivyo si vyema tu kusafirisha ikiwa ghafi ni bora kuiongezea thamani ili faida yake iwe ni kubwa zaidi na kuleta tija zaidi katika nchi.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali la kwanza, kwa sababu ni Sera ya Serikali kuunganisha mikoa kwa barabara ambazo ndizo tunazitegemea kwa ajili ya maendeleo yetu. Ni lini tutegemee Serikali itaunganisha barabara inayotokea Liwale Mkoa wa Lindi kuweza kufika Morogoro?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa muda mrefu sana Serikali imekuwa ikijificha kwa kusema kwamba kumekuwa na upembuzi yakinifu ukiwa unafanyika na mara nyingi upembuzi huu umekuwa ukichukua muda mrefu na wakati mwingine inaweza kufika hata miaka 10 tunakuwa kwenye upembuzi yakinifu. Ni lini tutegemee Serikali itaweza kuweka limitation au taratibu ambapo kutakuwa na muda maalum wa upembuzi yakinifu kufanyika ili ujenzi wa barabara uwe unaanza kufanyika mapema? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lathifah, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba ni Sera ya Serikali kuunganisha mikoa. Kama nilivyojibu wiki iliyopita wakati nikijibu swali la Mheshimiwa Mlinga, nilisema kwamba tutakwenda kutazama kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Lindi kwa maana ya Liwale na Mahenge, lakini hii ni siku za usoni, kwa sababu ziko logistics nyingi lazima zifanyike kwa sababu barabara hiyo itapita katika Hifadhi ya Selous lakini pia structures zake zinahitaji fedha nyingi. Kwa hiyo, tutaendelea kuitazama na Serikali inajua umuhimu wa kipande hiki cha barabara kuunganisha kuja Mahenge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kwamba Serikali inajificha kwa kusema inasanifu na kutengeneza michoro; hili siyo kweli. Niseme kwamba mpaka sasa hivi barabara za lami zinazounganisha mikoa karibu mikoa yote tunakamilisha. Barabara zaidi ya kilometa 13,000 tumeshatengeneza kwa lami kwa maana ya kuunganisha mikoa na nchi za jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata katika bajeti hii ya mwaka 2018/2019, tumependekeza kufanya usanifu wa barabara kilometa 3,856. Hizi ni kilometa nyingi sana na hii ni kuonesha jinsi namna gani Serikali ya Chama cha Mapinduzi iko committed kuhakikisha kwamba kila tunapokamilisha barabara fulani ni mwanzo wa kuendelea kusanifu barabara nyingine. Kwa hiyo, Mheshimiwa Lathifah ataendelea kusikia tukisanifu na kutengeneza michoro ya barabara kila wakati kwa sababu kila wakati tunavyokamilisha ujenzi wa barabara, kwetu sisi kama Serikali ni fursa ya kutengeneza barabara nyingine. Ahsante sana.