Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Deo Kasenyenda Sanga (45 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue nafasi hii kuungana na wenzangu kuunga mkono bajeti ya Waziri Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mjadala ambao ulikuwa unaendelea humu ndani wako watu waliosema hakuna utawala bora, Rais anaingilia mihimili mingine, mimi niseme, hivi wewe ndiyo baba mwenye nyumba, mke uliyemuoa ana watoto amekuja nao...
MHE. DEO K. SANGA: ...amezaa na mtu mwingine na mtu mwingine, wewe ndiyo wa tatu…
MHE. DEO K. SANGA: Unasimamia watoto wa kwako na hawa, hivi hawa wengine wakiwa wezi huwezi kuwaambia acheni wizi?
MHE. DEO K. SANGA: Utaambiwa unaingilia? Ndugu zangu, kwa nini tunadhoofisha nguvu zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano?
Rais anafanya kazi nzuri sisi sote ni lazima tukubaliane kwamba Rais anafanya kazi nzuri. Mawaziri wake wanafanya kazi nzuri ni lazima tuwaunge mkono, tumeona kwa macho yetu wenyewe. Halafu tunakuja hapa tunasema anaingilia mhimili mwingine. Hivi mtu unakuwa mwizi asiseme kwamba jamani acheni wizi? Hawa Ofisi yako Waziri Mkuu na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli lazima waangaliwe vizuri watumbuliwe na wenyewe. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya CCM…
MHE DEO K. SANGA: Kila wakati mmesema Serikali hii hakuna chochote, hakuna kitu, sasa imeleta bajeti tangu mimi nimekuwa Mbunge hakuna bajeti nzuri na yenye mwelekeo mzuri kama hii, hii sasa imebaki ni ukombozi kwa Watanzania. Tuseme kweli jamani, tuwe wapenzi wa Mungu bajeti hii ina mwelekeo mzuri, inaonesha dira kwamba sasa angalau wananchi wetu matatizo mbalimbali yatapungua au yatakwisha kabisa katika miaka mitano, lazima tuipongeze Serikali ya CCM.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie sasa Jimbo langu la Makambako. Rais alipotembelea katika mji wetu wa Makambako aliahidi ahadi sita na moja kutatua tatizo la maji katika mji wa Makambako.
Pili ilikuwa ni lami kilometa sita katika mji wa Makambako; tatu ilikuwa ni fidia ya soko la kimataifa kulipwa kwa wananchi wa mji wa Makambako na nne ilikuwa ni vifaa vya upasuaji katika hospitali ya mji wa Makambako.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mji wa Makambako tumepata madaktari wazuri, tatizo kubwa tunalolipata gari letu la kubebea wagonjwa kila siku linapeleka mara tano, mara sita Wilayani Njombe kwa ajili ya upasuaji. Tuombe sana Serikali itupe vifaa vya upasuaji ili kupunguza gharama za kupeleka watu kule Njombe kila wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tano, ni kuimarisha uwanja wetu wa michezo na sita ilikuwa ni umeme vijijini. Ahadi hizi zote za Rais nimewapelekea Mawaziri wote wanaohusiana na Wizara hizi. Ombi langu wahakikishe wanazifanyia kazi ili ziendane na kasi ya Rais wa Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, pale Makambako upande wa Polisi ni Wilaya inayojitegemea Kipolisi, yupo OCD na kadhalika. Tuna eneo kubwa sana la kujenga nyumba za polisi hata nyumba moja ya polisi pale haijajengwa. Ombi langu tuhakikishe tunajipanga vizuri ili tuweze kuwajengea nyumba nzuri za kuishi hawa askari wetu wa polisi pale Makambako.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jambo lingine upande huo huo wa polisi, katika kituo chetu pale ni centre kubwa sana ya kwenda Mbeya, Songea, Liganga na kadhalika. Gari la polisi linalotumika ni la siku nyingi na wakati fulani RPC amekuwa akitoa gari kutoka Njombe. Niombe sana tuhakikishe pale tunapewa gari na wakati fulani gari lingine limechukuliwa kutoka Ludewa na ndiyo lipo pale Makambako. Kwa hiyo, niombe sana katika bajeti hii kuhakikisha tunapata gari letu la polisi ili gari la Ludewa liweze kurudi Ludewa mahali ambapo walikuwa wameliazima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sera yetu inaelezea kujenga VETA kila Wilaya. Naomba tuhakikishe tunajenga VETA katika Wlaya yetu ya Njombe ili vijana hawa wanaomaliza darasa la saba, kidato cha nne waweze kwenda kujifunza ujuzi mbalimbali katika eneo letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe sana Waziri wa Ujenzi, tulikuwa tumeleta maombi kupitia kikao chetu cha RCC cha Mkoa kupandisha hadhi za barabara inayotoka Makambako – Mlowa - Kifumbe - Kitandililo na barabara nyingine ya TANROAD ambayo inatoka Ikelu - Ilengititu – Kifumbe. Niombe sana kwa sababu Halmashauri haina uwezo wa kuweza kutengeneza barabara hizi tuombe zipandishwe hadhi ili kusudi ziwe zinapitika wakati wote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, unajua bajeti hii hata kuchangia ni wajibu wa kuchangia lakini kama nilivyosema ni nzuri, ni lazima tuiunge mkono ili Serikali iende ikafanye kazi.
kwa sababu ya Serikali ya Awamu ya Tano na watu wanaomsaidia Rais Waheshimiwa Mawaziri, songeni mbele msisikilize maneno ya watu hawa, wanataka kuchelewesha shughuli za maendeleo. Hawa wamejipanga kuchelewesha shughuli za maendeleo ili 2020 tukwame, songeni mbele na watakwama wao. (Makofi)
Sasa umekuja hapa hutaki kuchangia na watu wamekutuma hapa uje kuchangia maana yake nini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi niseme tu nimalizie kwa kusema naunga mkono bajeti hii naitaka Serikali kuhakikisha tunapotoka hapa inakwenda kufanya kazi zilizopangwa katika maeneo yetu, CCM!
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie angalau kwa dakika tano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Waziri mwenye dhamana, Naibu Waziri, Watendaji wote wa Wizara hii ya Elimu, wanafanya kazi nzuri, mwelekeo tumeshauona nadhani tumeuanza vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Walimu wa Sayansi ambao Wabunge wenzangu wamelizungumzia sana. Sasa tatizo ambalo naliona, bila kuona namna gani tutalitaua, tutaendelea kuwa na tatizo na Walimu hawa wa Sayansi. Kwa mfano, Walimu hawa kila mwaka wanaopatikana ni wachache; na tatizo kubwa ambalo linajitokeza ni kwamba baadhi ya sisi wazazi; Walimu wenyewe tunawajengea mazingira watoto kwamba somo hili ni gumu. Hili ndiyo tatizo! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hebu tuone namna gani tunaanza kujenga misingi huku chini kutoka Shule za Msingi mpaka Sekondari kuona watoto wanapenda somo hili. Tukitengeneza vizuri watoto walipende somo hili, tutamaliza tatizo la Walimu wa Sayansi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumzia suala la shule binafsi. Shule za watu binafsi, naweza kusema ni sawa na hospitali za watu binafsi ambazo zinahudumia na Serikali inapeleka ruzuku pale. Hata Mwalimu Nyerere wakati ameanza kuambia Taasisi mbalimbali… (Makofi)
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Mwalimu Nyerere wakati anaanzisha shule za watu binafsi, Taasisi za kidini na kadhalika, ilikuwa ni kuisaidia Serikali. Kwa hiyo, nadhani sasa muda umefika, tuone namna ya kusaidia shule hizi kwa sababu na zenyewe zinatoa huduma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi Shule za Sekondari ambazo tumezianzisha katika Kata mbalimbali, Serikali imefanya kazi nzuri; tusimamie, ziboreshwe zilingane na hizi na baadaye hizi zitajifuta pole pole zenyewe. Hii ya kuelekeza kwamba kuwe na ada elekezi, sioni kama tutakuwa tunafanya kazi vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo linguine ni suala la Walimu. Kwenye Halmashauri yangu ya Mji wa Makambako, nilikuwa nadhani TAMISEMI Wizara hii ya Elimu, hebu tuone namna hii ya kuhakiki madeni haya haraka ili Waalimu hawa waweze kupewa stahiki zao. Wenzangu wengi wamesema hapa, Walimu wanafanya kazi nzuri sana; sasa tuone namna ya kuhakiki madeni haya ili waweze kulipwa stahiki zao haraka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo haya, nirudie tena, shule za watu binafsi zinafanya kazi nzuri, Serikali, isaidie kabisa. Zinafanya kazi nzuri sana. Tuwatie moyo! Mwaka 2015 shule hizi za watu binafsi zimefanya kazi vizuri, zimetoa watoto waliofaulu sayansi vizuri. Sasa kwanini tusiziunge mkono? Kwa nini tusiwasaidie?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii ya Waziri wa Elimu asilimia mia moja kwa mia moja, baada ya kuona haya marekebisho ya ada elekezi yaondolewe. Nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru na mimi kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze sana Wizara hii, watendaji wote na Waziri na Naibu Waziri, wamefanya kazi nzuri na bajeti hii ina muelekeo mzuri; wapate fedha, sisi tunasubiri maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu mmoja alikuwa anachangia jana hapa, anasema daraja la Kigamboni halina faida, hivi kweli halina faida daraja la Kigamboni, kweli? Ila amesema amekwenda mara nane, mara ngapi, anakwenda na kurudi, si ndio faida yenyewe. Kama daraja halipo angekwendaje? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano ni kwa ajili ya watu wa chini. Na watu wa chini kule, hivi tunakwenda kuwaambia leo mambo hayo watu wa Kigamboni kweli? Eeh, wanatembea kwa mguu, si ndio wana faidi daraja hili. Songa mbele Waziri, usirudi nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanazungumzia habari ya kuuza zile nyumba. Nyumba ziliuzwa Waziri Mkuu alikuwa Mheshimiwa Sumaye. Mheshimiwa Sumaye ndiye aliesimamia mambo hayo, ndiye alieuza zile nyumba, lakini na nyumba zile na nyumba…
MHE. DEO K. SANGA: …mnanijua, wee!
Mheshimiwa Mwenyekiti, na nyumba zile…
Mheshimiwa Mwenyekiti, na nyumba zile walionunua ni Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ni Mheshimiwa Sumaye, si athibitishe!
Mheshimiwa Mwenyekiti, walinunua nyumba zile ni Watanzania, ndio walionunua zile nyumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri mwenye dhamana, pale mjini…
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Waziri katika bajeti aone namna ya kutafuta fedha hata kilometa moja na nusu Makambako Mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, katika kupandisha daraja barabara za Halmashauri kwenda TANROADS, kuna barabara ya kutoka Makambako - Kifumbe, kutoka Usetule kwenda Kitandililo, tafadhali sana. Lakini vinginevyo Rais wa Awamu ya Tano…
MWENYEKITI: Ahsante! Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naungana na wachangiaji wenzangu kwanza kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu; Waziri Mkuu; Makamu wa Rais; Mawaziri na Waziri mwenye dhamana hii ya afya, pamoja na Naibu na Watendaji wake wote, kwa namna ambavyo wameonesha vizuri mwelekeo wa bajeti hii kwa mwaka wa 2016/2017. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwe wakweli. Unajua wakati fulani vijembe hivi! Hivi kweli pale Muhimbili hakuna mabadiliko! Muhimbili ukienda sasa hivi pana mabadiliko makubwa kabisa. Duka la MSD Mheshimiwa Rais alisema litakuwa pale, Waziri mwenye dhamana amesimamia liko pale. Vitu vingine, kuna mabadiliko makubwa! Kwa kweli tuwatie moyo kwa kazi nzuri mnayoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi kuna mchangiaji mmoja alizungumzia lugha fulani iliyokuwa inagusa akinamama. Akinamama wametuzaa; kalipuka! Ni mama zetu hawa, wametuzaa, lakini mmoja vile vile siku ya nyuma yake pia naye alidhalilisha akinamama hawa hawa! Alitamka kwamba alipokwenda huko wakapigwa, wakakatiwa shanga zao. Hivi ndiyo vya kuzungumza hapa vitu nyeti kama hivyo? Eeh! Sasa niseme, kama Mwenyekiti wa CCM mwenzangu kwa yule kijana ambaye Mbunge alizungumzia lugha ambayo CCM hatukumtuma, mimi namwombea radhi kama Mwenyekiti. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tuliopo hapa, kila mmoja ana akili; na wakati fulani tuliopo hapa wote ni vichaa, lakini vichaa vinatofautiana. Ukienda upande wa elimu na ndiyo maana sekondari, shule za msingi na kadhalika huwa kunakuwa na shule za watu wenye vipaji maalum. Maana yake hawa wana akili kuwazidi wenzao. Sasa baadhi ya Wabunge hapa walizungumzia habari ya viti kumi ambavyo Mheshimiwa Rais anawateua kwa kazi maalum, kwa vipaji maalum. Ndiyo maana alimteua Mheshimiwa Tulia, Naibu Spika kwa kazi maalum. Kwa hiyo, tusimwingilie Mheshimiwa Rais, kazi ambazo anawateua watu, zile nafasi kumi amemteua Waziri wa Fedha, ameteua na wengine, tusimwingilie nafasi zile kumi. Hata Mheshimiwa Mbatia amewahi kuteuliwa kupitia Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie habari ya Jimbo la Makambako. Nilimwandikia Mheshimiwa Waziri ile ahadi ya Mheshimiwa Rais. Ndugu zangu, naishukuru Serikali, miaka miwili, mitatu iliyopita mmepandisha hadhi Kituo cha Makambako kuwa hospitali na mmetuletea Madaktari wa kutosha, tunao. Tatizo kubwa nimekuwa nikisema hapa na niliseme tena kwa Mheshimiwa Waziri, tuna jengo la upasuaji, tulichokikosa ni vifaa vya upasuaji. Gari letu la wagonjwa limekuwa likipeleka watu Njombe kila siku, mara saba, mara tano mpaka mara nane. Ni gharama kubwa!
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha na nilimltea, akaniambia Daktari anipe orodha ni vitu gani vidogo vidogo ambavyo vimekosekana. Nilimpa! Atakapohitimisha aniambie wamejipangaje kuona sasa tunapeleka vifaa vya upasuaji pale Makambako ili kuwaokoa akinamama na watoto, gari lisiwe linakimbia kwenda Njombe na Ilembula. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo hospitali yetu ya Makambako tuna wodi ya akinamama na watoto. Wodi nzuri iliyojengwa zaidi ya miaka miwili, vimebakia vitu fulani fulani havijakwisha; miaka miwili tume-invest pale hela ya Serikali. Nawaomba Wizara waone uwezekano wa kuona tunamalizia jengo hili ili liweze kufanya kazi iliyokusudiwa. Chonde chonde, ili kuokoa hela ya Serikali ambayo imeendelea kukaa kwenye majengo hayo mawili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kufungua maduka ya MSD katika hospitali zetu za mikoa na wilaya, naomba sana, Mkoa wetu wa Njombe ni mpya. Mkoa huu ndiyo Mkoa ambao sasa una kitega uchumi kikubwa ambacho kitaanzishwa, Liganga na Mchuchuma. Kwa hiyo, naomba sana tuhakikishe tunapeleka Duka la MSD la Madawa pale Mkoani Njombe ili kuwasaidia wananchi wetu wa Wilaya na Mkoa wa Njombe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Halmashauri ya Mji wa Makambako tumejenga zahanati tisa katika vijiji tisa; na karibu zahanati saba tumeshazipaua. Naomba Serikali ione upo umuhimu sasa wa kutenga bajeti ya kumalizia kuwaongezea nguvu wananchi hawa wa Mji wa Makambako. Hili linawezekana na ni kwa nchi nzima. Yako majengo ambayo yamejengwa hayajamalizika, tunaomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya kumalizia haya majengo ambayo yalishajengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tuna Kituo cha Afya ambacho kilijengwa katika Kata ya Lyamkena. Kituo hiki cha Afya kina zaidi ya miaka miwili. Kilishapauliwa na kadhalika, bado hakijamaliziwa, kimeendelea kukaa pale. Jengo hili la kituo cha afya, inawezekana kabisa na majimbo mengine vituo vya afya kama cha Makambako, vipo! Tutenge fedha kwa ajili ya kumalizia vituo vya afya ili kazi iliyokusudiwa iweze kwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana kwa kasi anayokwenda nayo ambapo yuko nyuma ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, imani yangu na imani ya Wabunge hawa, atatufikisha salama. Nampongeza sana kwa dhati pamoja na Watendaji wake. Kwa hiyo, ni imani yangu kwamba haya ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyasema, atakapokuwa anahitimisha, basi ni vizuri atueleze kwa ujumla wake ili tuweze kuwa kitu kimoja na CCM ahadi ambazo iliahidi, tunamtegemea yeye kupitia Wizara hii ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo haya, nisiwachukulie muda wenzangu, niseme tu naunga mkono hoja ya Waziri wa Afya kwa asilimia mia moja. Nawashukuru sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Wanasema ukiona watu wanasema wewe una tatizo, wewe songa mbele, wewe ni jembe unafaa kutumikia wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutuletea bajeti nzuri yenye mwelekeo na kwa kumteua Waziri Mpango pamoja na Naibu Waziri. Naipongeza Wizara ya Fedha na Watendaji wote kwa kutupa bajeti yenye mwelekeo mzuri kwa maendeleo ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mategemeo yetu Watanzania ni kwamba matatizo ya maji, elimu, afya, barabara, umeme yatapungua. Hii ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa ahadi alizozitoa Mheshimiwa Rais kwa Watanzania ikiwemo Mji wa Makambako ambapo aliahidi maji, vifaa tiba, lami kilomita sita, umeme na kadhalika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, imani yangu bajeti hii hata waliotoka humu ndani nao wanahitaji maendeleo kwenye Majimbo yao. Rais wetu alishasema maendeleo hayana chama, peleka maendeleo hata huko katika Majimbo waliyotoka utakuwa unawatendea haki Watanzania. Ingawa wenzangu watasema, aah, aah, ndugu zangu tunawapelekea maendeleo Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala hili ambalo limeleta mkanganyiko mkubwa juu ya mageti ambayo yalishatangazwa kwamba yanaondolewa kwenye Halmashauri zetu yanayohusiana na ushuru. Waziri atakapokuwa anahitimisha hapa atuambie jambo hili limekaaje maana tayari linaleta mkanganyiko kuhusiana na kuondoa mageti haya ya ushuru wakati Halmashauri zilishaweka bajeti na wananchi wameshapata kauli ya kwamba ushuru sasa umeondolewa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Waziri kwa kuondoa tozo mbalimbali kwa wakulima. Jambo hili limeleta faraja kubwa sana kwa Watanzania na wakulima wetu. Nirudie tena kumpongeza Rais John Pombe Magufuli kwa kumteua Waziri huyu Mheshimiwa Dkt. Mpango sasa tunaona mipango itakwenda vizuri, nakupongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napingana na hawa watu ambao wametoka hapa na wamekuwa wakipinga kwamba hii bajeti haina mwelekeo na kadhalika, ndugu zangu uchaguzi ulishakwisha, Rais sasa ni Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu, Waziri Mkuu ni Mheshimiwa Majaliwa Majaliwa pamoja na Mawaziri wote walioteuliwa, naomba chapeni kazi ya maendeleo kwani watu wanasubiri maendeleo katika maeneo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wengi wamezungumzia sana suala la kiinua mgongo. Mimi niseme tu kwamba suala la kiinua mgongo linagusa Watanzania wote hasa watumishi. Watumishi pamoja na Waheshimiwa Wabunge tumekuwa tukikatwa kodi mbalimbali lakini kodi hii ya kiinua mgongo kwa watumishi nadhani iangaliwe upya. Kwa sababu watumishi hawa wametumikia nchi na wamekatwa kodi mbalimbali. Kwa hiyo, naomba suala la kiinua mgongo kwa watumishi wote kwa ujumla liangaliwe vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze Serikali imesikia kilio cha Wabunge ambao wamezungumzia sana suala la manunuzi kwamba lilikuwa ni tatizo kubwa katika Halmashauri zetu na wenzangu wengi wamesema hapa. Suala hili la manunuzi ilikuwa hela zikipelekwa kwenye Halmashauri zinaliwa tu na baadhi ya watendaji ambao siyo waaminifu. Naishukuru sana Serikali, Waziri alisema hapa unaletwa Muswada wa kubadilisha Sheria ya Manunuzi na mimi naafiki kwamba utaratibu huu ukibadilishwa utaleta tija na maendeleo katika Halmashauri zetu na hizi fedha zote zinazojadiliwa hapa sasa zitakwenda kutumika ipasavyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wetu wa Makambako sasa tunazungumzia suala la kujenga viwanda, watu wanahitaji kuwekeza viwanda katika mji wetu lakini tatizo kubwa ni upatikanaji wa maji. Niipongeze sana Wizara ya Maji ambayo tayari imetenga fedha kwa ajili ya kutatua tatizo la maji katika Mji wa Makambako. Kwa hiyo, tunaomba Wizara ya Fedha ipeleke haraka fedha hizi ili ziweze kuleta maji ili wawekezaji waweze kuanzisha viwanda katika Mji wetu wa Makambako. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, hili nimelisema mara nyingi sana, naomba nirudie, Serikali imewekeza fedha kwenye hospitali yetu pale kwa miaka zaidi ya minne sasa, tumejenga wodi mbili kubwa za akina mama na watoto imebaki tu kumalizia, miaka minne imebaki magofu. Mheshimiwa Waziri wa Fedha hebu liangalie suala hili zinahitajika hela kidogo sana ili wodi hizi ziweze kufanya kazi iliyokusudiwa kwani fedha ya Serikali imekaa pale kwa muda mrefu. Namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha aone ni namna gani atatatua tatizo hili la kumalizia wodi hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kwamba hospitali ile ya Mji wa Makambako imeshapandishwa hadhi na kuwa hospitali kamili na kwa miaka mitatu tunakwenda vizuri. Tatizo ambalo lipo katika Mji wetu wa Makambako, nilimueleza hata Waziri wa Afya na Waziri wa TAMISEMI, tayari tuna jengo pale la upasuaji ambalo limeshakamilika lakini tunakosa tu vifaa tiba vya upasuaji. Tuna gari letu la ambulance kwa siku mara saba linapelekea wagonjwa Njombe kwa ajili ya upasuaji. Fedha inayohitajika ni kidogo sana hata shilingi milioni 30 hazifiki ili tuweze kununua vifaa vya upasuaji vilivyobakia ili shughuli za upasuaji ziweze kuendelea. Mmetuletea Madaktari wazuri wako pale wamekaa tu hawawezi kufanya kazi kwa sababu shughuli za upasuaji hakuna. Namuomba Waziri wa Fedha atakapokuwa anahitimisha aone namna ya kutatua tatizo la kununua vifaa vya upasuaji ili kuweza kutatua tatizo la Makambako. Vifaa vinavyohitajika ni kifaa cha kuchanganyia dawa ya usingizi na vitu vidogo vidogo tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo yote naungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu, Waziri Dkt. Mpango chapa kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia 100. Ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia mpango huu ambao umeletwa mbele yetu. Mpango huu ni mzuri sana, una mwelekeo mzuri na dira nzuri ya kuhakikisha shughuli zote ambazo zimepangwa hapa zinakwenda vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua hata vitabu vitakatifu vinasema unapotaka kwenda peponi au mbinguni ni lazima ukeshe ukiomba. Sasa kazi ya kukesha na kuomba si ndogo, ni kubwa sana, kazi ya kukesha na kuomba na ukishakesha na kuomba ndio unaweza kufika peponi au mbinguni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii ya Awamu ya Tano kazi kubwa ambayo ilikuwa ikiifanya ni kuturudisha kwenye mfumo, kuachana na ule utaratibu tuliouzoea kwa hiyo, ilikuwa inaturudisha kwenye mfumo. Turudi tujenge nidhamu katika Serikali na kazi hiyo imefanywa na Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, amefanya kazi nzuri sana. Hata wakati anawaambia Watanzania anaomba ridhaa aliyasema haya kwamba, nipeni nitafanya moja, mbili, tatu; leo anayafanya haya tunasema aahhaa, anafanya vibaya! Lakini mtu mmoja amewahi kusema ukiona mtu anakusifia jiangalie mara mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi inayofanywa na Serikali kupitia Mawaziri waliopo na huyu ambaye ameleta mpango huu ni kazi nzuri sana. Sasa kwamba Serikali imeturudisha kwenye mfumo, imedhibiti mambo ya pesa, Mheshimiwa Mpango baada ya kudhibiti sasa peleka kwenye Halmashauri ili zikafanye kazi, maana kwanza alikuwa anaturidisha kwenye mfumo na sasa tumerudi kwenye mfumo, kwa hiyo fedha sasa zianze kwenda kwenye Halmashauri ili zikafanye kazi iliyokusudiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu waliozungumzia habari ya Liganga na Mchuchuma. Na mimi napata ukakasi, hivi kuna tatizo gani linalofanya shughuli ya Liganga na Mchuchuma ikwame? Kwenye mpango imekaa vizuri, tunaomba Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana suala la Liganga na Mchuchuma hebu sasa liweze kusonga mbele kadri ambavyo lilikuwa limepangwa ili liweze kusaidia Tanzania, tuweze kupata ajira nyingi kwa vijana wetu wa Tanzania kama ambavyo mpango upo vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua napata taabu kitu kimoja kidogo sana! Mambo mengi amenimalizia yuko pale, ambayo nilikuwa nimeyaweka hapa kwa sababu...! Sasa naomba niseme! Eeh, ndio mwenyewe! (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani wote ni Wabunge sawa, kila mmoja ana hadhi yake ameingia hapa, tunahitaji kuheshimiana. Tunapomnyooshea mtu, Mbunge mwenzako kwamba eti wewe huoni uchungu kwa sababu uliteuliwa, tena huyu ndiye anaheshima kubwa sana kuliko wewe, kwa sababu kama alivyosema Mbunge mwenzangu pale kwamba kila mmoja amepata kura kwa idadi tofauti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nani aliyepata humu ndani kura nyingi kama za Mheshimiwa Magufuli, nani? Sasa zile zote si ndio amepewa yule kwa heshima ya Watanzania? Ndugu zangu tuheshimiane, aliyeteuliwa, ambaye hakuteuliwa wote ni Wabunge. Wakati fulani ninyi wenyewe ndio mnatoka huko mnakwenda pale, Waziri eeh, moja, mbili, tatu! Ni Waziri huyu, apewe heshima yake kama ambavyo Wabunge wengine tuko hapa ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya kudhibiti mambo yote sasa peleka fedha Halmashauri zikalipe na fidia zile pamoja na Makambako ikiwemo. Kuna fidia kule wananchi wangu wanadai kule ili zikaweze kufanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla mpango huu nauunga mkono vizuri, ni mpango mzuri ambao sasa peleka fedha zikaanze kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sina la ziada. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza kwa kazi nzuri sana zinazofanyika katika nchi hii ya Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli pamoja na Waziri na Naibu Waziri na watendaji wa Wizara. Ombi, pamoja na bajeti nzuri ikiwemo barabara za Mji wa Makambako kilometa sita za lami; naomba kujua mradi wa kujenga One Stop Center lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, utaanza pale Idofi maana watu hawa wamekuwa wakisubiri muda barabara kutoka Ilunda – Igongolo urefu wa kilometa tisa ni ya TANROADS mbele inaendelea Kifumbe - Mahongole mpaka Makambako urefu wa kilometa 19. Ombi, iunganishwe iwe kuanzia Igongolo kuwa TANROADS.

Mheshimiwa Naibu Spika, mawasiliano Lyemukena – Majengo - Kifumbe, Kitandilo-Mahongole hakuna mawasiliano, tunaomba mawasiliano
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niungane na wenzangu kuweza kuchangia. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Waziri pamoja na Naibu Waziri na Katibu Mkuu na Manaibu pamoja na Wizara nzima kwa kazi nzuri wanayowatendea haki Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimpongeze Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwaamini hawa ambao wanawatendea Watanzania wanakwenda kwa kasi. Nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na miradi kadhaa ya maji katika Jimbo la Makambako. Nimeona kwenye bajeti wametutengea fedha, ombi langu Mheshimiwa Waziri na kundi lako, pale Ikelu pana mradi unaoendelea, mkandarasi yuko pale. Ombi langu tunaomba mkandarasi huyu kwasababu amesimama na yuko hatua za mwisho, mumlipe fedha ili aweze kumalizia mradi wananchi wa Ikelu waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile tuna mkandarasi yuko pale Ibatu. Mkandarasi huyu amesimama kwasababu hamjamlipa fedha. Tunaomba alipwe fedha ili kusudi aendelee kukamilisha ule mradi ili wananchi wa Ibatu waendelee kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna mkandarasi yuko pale Usetule Mahongole, vilevile amesimama. Niombe sana Mheshimiwa Waziri na timu yako tuhakikishe tunawalipa ili wamalizie kwasababu, wamebaki hatua za mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mkandarasi wa mwisho yuko pale Nyamande, Mbugani na Mtulingala, Mkandarasi huyu anafanya kazi nzuri, lakini amesimama hawezi kuendelea kwasababu, hajalipwa fedha. Niombe sana aweze kulipwa fedha ili aweze kumalizia kazi iliyokusudiwa wananchi wale waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niungane na Wabunge wenzangu, tuna miradi ile ya miji 28. Katika miji 28 ikiwepo na Makambako. Na katika Makambako kuna kata tisa zinazotegemea mradi huu au miradi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba utakapokuwa unahitimisha hapa uwaambie wananchi wa Makambako ni namna gani wana imani kubwa ingawa katika maelezo yako umeeleza vizuri tumepata imani kwamba, mradi huu sasa unakwenda kutekelezwa. Sasa kwenye hitimisho hapa useme ili wananchi wa Makambako waweze kupona; wajue katika kata zao tisa wanazosubiri katika mradi huu mkubwa ni lini mkandarasi atakuwa katika Mji wa Makambako ili wananchi wa Makambako waweze kupata maji? Na wakati huo unapohitimisha na hii niliyoisema ya makandarasi waliosimama nayo useme hapa, ili wananchi wa Makambako wapate imani kama ambavyo ulituambia kwenye kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa leo nilitaka nizungumzie hili ambalo wakandarasi hawajalipwa na hii miradi ambayo ya miji 28. Watu wana imani kubwa sana ya miji hii 28 hasa ukiwepo na Mji wa Makambako ambao wananchi wanausubiri kwa hamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, ahsante sana.
(Makofi)
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Kwanza nizungumzie suala linalohusiana na maji. Kwenye bajeti ya kipindi kilichopita kuna miradi mikubwa ambayo tuliipitisha hapa. Kwa mfano, kuna miradi mikubwa ya maji ya miji ya Makambako, Njombe na Wanging’ombe ambapo ilionyesha fedha zinatoka Serikali ya India. Kwa hiyo, ni vizuri Waziri atakapokuwa anasimama atuambie Serikali imejipangaje juu ya kutatua tatizo la maji kwa mradi mkubwa huu wa Makambako, Njombe na Wanging’ombe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni suala la pembejeo hizi za ruzuku ambapo Mkoani kwetu Njombe zinachelewa sana. Sisi tunaanza kupanda kuanzia mwezi wa 11 na kuendelea. Kwa hiyo, Serikali ijipange vizuri msimu huu tunaokwenda sasa kuona kwamba pembejeo hizi zinafika kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la tatu, kuna hawa wasambazaji ambao mpaka sasa wanaidai Serikali na mpaka sasa wako watu ambao wamefilisika, wako watu wanauziwa nyumba zao. Ni lini Serikali italipa deni hili ambalo wananchi hawa walisambaza pembejeo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la nne, ni suala la lumbesa kwa wakulima, nadhani Serikali ijipange vizuri suala hili lipigwe marufuku kwa nchi nzima ili kusudi isiwaumize wakulima.
Mheshmiwa Mwenyekiti, jambo la tano ni mifugo. Suala la mifugo limekuwa ni tatizo kubwa sana kwa wafugaji na wakulima na watu wanapoteza maisha. Aidha, Kamati au ninyi Serikali muone namna ambavyo nchi ya Sudan wana mifugo mingi kuliko sisi lakini hakuna tatizo la wakulima na wafugaji, waende kule wakajifunze wenzetu kule wanafanyeje mpaka hakuna migogoro ambayo ipo kama huku kwetu kila wakati mara watu wameuawa na kadhalika. Kwa hiyo, nadhani Serikali ijipange kuona namna ya kuondoa tatizo hili la mifugo na wakulima kwa sababu limekuwa ni kubwa sana, siyo kitu kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la sita, hapa kuna watu wamezungumzia Wizara hii ya Kilimo. Mimi niseme ndugu zangu, Waziri huyu Tizeba na Naibu wake wakati fulani tunawalaumu bure tu, sasa watachukua wapi fedha kama hawana fedha? Nadhani sisi tuungane kwa pamoja kuona namna ambavyo tunaiambia Serikali ili bajeti ya msimu huu tunaokwenda iwe nzuri kuliko bajeti iliyokwisha ambapo ilitengwa shilingi bilioni 20 tu ambazo hazijatosha kitu chochote.
Kwa hiyo, nilikuwa nadhani sasa badala ya kumlaumu Waziri na Naibu wake na Wizara kwa ujumla, tuone namna ambavyo sasa Serikali inajipanga kuona msimu huu tunakuwa na bajeti ya kutosha kwa sababu ndiyo uti wa mgongo kwa wakulima wetu. Nadhani tukifanya hivyo, Serikali ikiongeza bajeti tutakwenda vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mengi lakini kwa sababu na mimi nipo kwenye Kamati hii nirudie tena kuzungumzia hili suala la maji, Waziri utakaposimama uwaambie wananchi wa Makambako wataondokana lini na tatizo kubwa hili la maji na uwaambie fedha za kutoka nje wananchi wale wa Njombe, Wanging’ombe wanazipataje na mpango huu sasa unaendeleaje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2016
MHE. DEO K. SANGA:Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, naipongeza sana Serikali kwa kuleta muswada huu ambao Wabunge wameelezea kwa muda mrefu sana ili kuleta tija na mabadiliko makubwa ambayo huko nyuma lilikuwa ni tatizo kubwa sana. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kupitia Waziri wa Fedha, Naibu na watendaji wote wa Wizara hii ya Fedha ikiongozwa na Mheshimiwa Mpango.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli lilikuwa tatizo kubwa sana tulifika mahala unakuta bati moja lilikuwa linaweza kununuliwa kwa shilingi 35,000; simenti shilingi 22,000; mimi ninasema hivyo iko haja ya kipindi kilichopita mimi kama Mbunge, Mfuko wa Jimbo tulinunua simenti kwa shilingi 22,000 na bati la geji 28 kwa shilingi 35,000; ukiuliza wanasema Sheria ya Ununuzi. Jamani mbona huko madukani wanauza bei chini? Sheria ya Ununuzi. Kwa hiyo nadhani sasa imeletwa wakati muafaka kabisa kwamba sasa tutaangalia soko linasema nini. Kwa hiyo mimi nadhani tutawatendea haki watanzania walipakodi na kadhalika.
Lakini pamoja na marekebisho hayo, nivizuri marekebisho hayo bado Serikali iendelee kuangalia mapungufu madogo madogo ambayo yataendelea kujitokeza ili waendelee kukaa na kuona namna ambavyo waweze kurekebisha uendelee mpango mzuri zaidi kadri ambavyo itakavyokuwa inakwenda. (Mkofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu Kamati ya Mipango na Fedha za Halmashauri, mimi nishauri na niombe sana, sijaona kama wameleta amendment hapa; lakini ni vizuri Kamati hizi hasa Kamati ya Mipango na Fedha ya Halmashari iendelee kama ilivyokuwa ni lazima angalu ipitie kwa sababu Kamati hizi zinakaa kila mwezi mara moja ili kuona kwenye Halmashauri yao ni kitu gani ambacho kimejadiliwa kwenye Bodi ya Zabuni. Sasa tukiondoa kabisa Kamati hii ya Mipango na Fedha na wao ndio wenye fedha za Halmashauri na bajeti hii ambayo tumeendelea kuijadili na kuimalizia sasa Serikali imetenga fedha nyingi kwenda huko, haki ya Mungu zitakwenda kuliwa, tutakuwa tulichokifanya hakipo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana kwamba waone uwezekano kabisa wa Kamati hii ya Mipango na Fedha kama alivyo Mpango mwenyewe Waziri wetu aone uwezekano wa kwamba Kamati hii ni vizuri ikapitia, itakuwa tumeitendea haki kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiuangalia muswada huu umelenga pia kuwa hudumia walemavu, jamii mbalimbali, akina mama, watoto na kadhalika, tumeutendea haki kabisa muswada huu nadhani umefika mahala pake ambapo sasa maelekeo ni mazuri.
Mimi niombe tu Waziri Mpango tunakuamini sana, Bunge hili linakuamini sana, wewe, Naibu wako pamoja na Wizara nzima, tuombe sana, Kamati ya Mipango na Fedha, niombe sana ishiriki kwenye mambo hayo ambayo wao watakuwa wamepitisha kule hawa wanapitia kuangalia kilichomo kwenye Halmashauri yao tutakuwa tumeitendea haki sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, vinginevyo naunga mkono hoja, ahsante sana, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti hii ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa uamuzi wake kwenye busara wa kuhamisha Wizara zote kuja Makao Makuu Dodoma. Pili, vile vile nimpongeze Waziri mwenye dhamana ndugu yetu Jenister Mhagama kwa kusimamia vizuri wizara hizi; zinaturahisishia sisi kama Wabunge kuweza kupita katika maofisi ambayo yako jirani, kwa hiyo tunaipongeza sana Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nianze na Wizara ya Afya; niiombe sana Serikali ione namna ya kuboresha maboma mbalimbali ambayo tumejenga huko kwenye majimbo yetu hasa zahanati na vituo vya afya ili yaweze kumalizika na kufanya kazi kama ambavyo sera inaelekeza
kuwa kila Kijiji na Mtaa kuwa na zahanati na kituo cha afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na kwenye Jimbo langu; mimi na Waheshimiwa madiwani wenzangu na Serikali tumeweza kujenga zahanati 13 na kituo cha afya kimoja kizuri sana ambacho kimesimamiwa na diwani mmoja anaitwa Mlumbe kutoka pale Yamkeno. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali ione namna ya kuboresha vituo hivi ili kusudio lile la kuwa na zahanati na Kituo cha Afya Kilonani iweze kutekelezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niishukuru sana Serikali kwa eneo langu la Makambako kwa kutupa vifaa vya upasuaji; naipongeza sana Serikali kwa namna ambavyo imetupa vifaa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maji. Naomba nipate majibu juu ya miradi ile mikubwa ya Miji 17 kwa Wizara hii ya Maji, fedha ambazo zinatoka India, katika miradi hii 17 mikubwa, mmojawapo upo katika Jimbo langu la Makambako. Kwa hiyo, naomba nipate majibu kutoka kwa Serikali, kwamba ni lini sasa fedha hizi zitakuja ili wananchi wa Makambako wawe na matumaini kwamba watapata mradi huu wa maji kama ambavyo Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba Waziri mwenye dhamana atakayemteua ataanza kuja Makambako na nashukuru sana Waziri alikuja kama
ambavyo Rais alisema.
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo. Niiombe Serikali ione namna ya kuboresha Wizara hii ya Kilimo hasa pembejeo hizi za ruzuku kwa sababu Serikali imekuwa ikipoteza fedha nyingi juu ya pembejeo za ruzuku. Nadhani Serikali ione namna ya kupunguza tozo na kodi mbalimbali hasa kwa pembejeo hizi za mbolea ili kusudi kila maduka yauze na mkulima aende kununua kwa bei ambayo ni ya chini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile Serikali ione namna ya kuboresha mbegu. Wako watu ambao wamekuwa wakifanya kazi ya kuchakachua hizi mbegu; wakulima wetu wanapopanda mbegu hizi zimekuwa hazioti. Niiombe sana Wizara kwamba ifufue maeneo ambayo
walikuwa wanapanda mbegu kama pale Uyole, Njombe tulikuwa na pale NDC, tuna maghala pale na mashamba walikuwa nayo, wafufue suala hili la pembejeo ili wananchi wetu waweze kupata. Kwa hiyo, suala la mbolea nimeshalizungumzia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu; niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, pamoja na kazi nzuri anayoifanya, ingawa wapo watu wengine hata ungefanya kazi watasema hakuna kinachofanyika; unajua mtoto wa kambo hata ungemlea namna gani atasema hakuna kazi
zinazofanyika; Waziri unafanya kazi nzuri kupitia Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana ndugu yangu Mheshimiwa Profesa Mbarawa kwamba katika ahadi zile za rais za kilometa sita za kujenga lami katika Mji wa Makambako, nikuombe sana na ile kilometa moja ambayo ulisema ingeanza mwaka huu wa 2016/2017 na muda
uliobaki ni mfupi, nimwombe sana Waziri ahakikishe kwamba, kilometa sita zile ambazo Rais alisema, mwaka wa 2017/2018 zinajengwa, ile ahadi itekelezwe ili wananchi wangu wa Makambako waweze kupata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, umeme. Nikupongeze sana Mheshimiwa Profesa Muhongo, Naibu Waziri wako pamoja na Serikali kwa ujumla kwa kazi nzuri ambayo tunaiona mnaifanya, hongereni sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nami niseme, kwenye jimbo langu, maana kipindi kilichopita ilikuwa nipate awamu ile ya pili ya REA; lakini yule mkandarasi ambaye mlinipa, Lucky Export na baadaye mkamwondoa, kwamba hakuwa anakidhi vigezo, sasa mmeniambia mnaniletea mwingine kutokana na majibu ambayo nilimuuliza hapa Naibu Waziri. Niombe sana ahakikishe safari hii mkandarasi huyo anakuwa site kule Makambako katika vijiji vile nilivyovitaja ili shughuli hii ya umeme wananchi wangu waweze kupata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, fidia. Waziri wa Viwanda yuko hapa na Waziri wa Fedha yuko hapa, Waziri Mkuu alipokuja Makambako aliwaona wale wananchi, yaani mimi Mbunge wao silali. Chonde chonde, niwaombe sana kuhakikisha kwamba tunawapa fidia wananchi hawa kwasababu wameteseka zaidi ya miaka 18. Nikuombe sana, fedha hizi kwa Serikali ni hela ndogo, ili tuhakikishe sasa; kwa sababu na kwenye Bajeti ya Mwaka 2016/2017 walishawekwa; nimwombe sana ndugu yangu Mheshimiwa Mpango tuhakikishe kwamba fedha hizi zinatolewa ili
wananchi wangu wa Makambako waweze kupata kama ambavyo Mheshimiwa Rais aliwaahidi kwamba jamani suala la fidia tutakwenda kulimaliza. Nimwombe sana na mimi namwamini sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, michezo. Ndugu yangu Mheshimiwa Mwakyembe uko hapa, Rais alituahidi kutuboreshea uwanja wetu wa michezo, nimwombe katika Mpango wake wa Bajeti ya Mwaka 2017/2018 ahakikishe anaweka bajeti kwa ajili ya kuanza kutengeneza uwanja wetu wa michezo pale Makambako.
Mheshimiwa Naibu Spika, elimu. Niipongeze sana Serikali, tangu ilipokuwa inatoa fedha kwa ajili ya elimu bure watoto wameweza kuongezeka na kadhalika, lazima tuipongeze Serikali kwa kazi nzuri. Tumwombe Waziri mwenye dhamana kuhakikisha mnapeleka vifaa vya maabara ili watoto wetu waweze kupata elimu yenye tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la fedha; tuhakikishe zinakwenda kwa wakati katika halmashauri zetu ili na sisi kama Madiwani tukiwa huko tuweze kusimamia zifanye shughuli za maendeleo kama ambavyo zimepangwa hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini liko jambo hapa lazima niliseme, nisipolisema hapa nitasema wapi. Wapo Wabunge wenzangu wamesema, hivi iko sheria gani inayosema wewe Mbunge kwa sababu una kinga ukiitukana Serikali usikamatwe, sheria ya wapi? Kama umeitukana Serikali ni lazima ukamatwe upelekwe kwenye vyombo husika ukahojiwe kwa nini umeitukana Serikali. Kwa hiyo tusiweke kama kinga kwa sababu tuna kinga basi tuitukane tu Serikali halafu tusikamatwe, mimi sikubaliani kabisa, lazima tukamatwe, chombo kinachohusika kitufikishe mahali panapohusika. Unajua wako watu walizoea Serikali iliyopita kazi yao ni kuitukana Serikali, lazima tukubaliane na mabadiliko! Wewe unaitukana Serikali wakuache tu, unapita unaitukana Serikali wakuache, haiwezekani! Haiwezekani! Serikali inafanya kazi nzuri, tunaona (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi nami niwe wa kwanza kuchangia katika hotuba hii ya Viwanda na Biashara. Kwanza nianze kwa kuishukuru Serikali ya CCM inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri wote na watendaji wa Wizara mbalimbali kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kutekeleza Ilani ya CCM. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepitia hapa hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, ukurasa wa 24. Hivi Mkuu wa Nchi ndiye baba, Rais, amepita mahali wananchi wamelalamika akatoa jibu kwamba atawasaidia, sasa hapa wanasema kwa nini alitoa majibu ya papo kwa papo kule wapi na nini, walitaka afanye nini? Watu wamemlalamikia Mheshimiwa Rais, si lazima ndio awape majibu wanasubiri na kwenye Ilani ya CCM tulisema tutatekeleza tutatoa majibu ya kuwasaidia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo vile vile Bunge lako hili tumesema kwamba kuna baadhi ya mikataba hasa ya madini sio mizuri tulisema hapa, sasa imetekelezwa tena tunalalamika tunasema kwa nini michanga na kadhalika, aaa. Serikali imeunda Kamati ya kushughulikia, tuiache Serikali ifanye kazi yake. Kwa hiyo naipongeza sana Serikali kwa kazi nzuri inayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie juu ya Wizara hii, juu ya fidia iliyoko katika Soko Kuu la Kimataifa katika Mji wetu wa Makambako. Kitabu cha bajeti, kilichopita cha 2016/2017, Serikali ilitenga fedha kwa ajili ya kuwalipa fidia wananchi wa Makambako na Mheshimiwa Rais alipopita pale aliwaambia fidia hii mtalipwa; na alipokuja Waziri Mkuu alisema majibu nitarudi nayo mimi ya kuwalipa fidia wananchi wa Makambako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kabisa Serikali ione maana kwenye kitabu hiki cha bajeti ambacho kiko hapa, cha 2017/2018 haipo tena, hazijawekwa. Kwa hiyo niiombe Serikali itekeleze na mwisho ni mwezi huu Juni, niiombe sana Serikali ihakikishe inalipa fidia za wananchi wa Makambako, vinginevyo mimi kama Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa leo nitashika shilingi kama nitakuwa sijapata majibu maana kwenye bajeti ya 2017/2018 hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali ihakikishe inalipa fidia ya wananchi katika maeneo ya Makambako. Wananchi hao wamekaa kwa muda mrefu, hawawezi kufanya kitu chochote wala kuendeleza wala kufanya kitu chochote katika maeneo yale na Serikali ilisema italipa fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri uko hapa na nilikutana na Waziri wa fedha akanihakikishia tutalipa fidia, nikuombe Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya viwanda uko hapa nimwombe ahakikishe wanasimamia kulipa fidia katika eneo hili la Makambako. Vile vile katika fidia, wako hawa watu wa ujenzi, kuna mradi unaojengwa pale, one stop center ambao unajengwa katika eneo letu la Makambako, vile vile nao wanahitaji kulipwa fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kupitia hili nimwombe sana wahakikishe wanawasiliana pia katika Wizara hii nyingine ambayo kuna fidia mbili hapo, kuhakikisha tunalipa fidia ya Mji wetu wa Makambako ili wananchi wa mji ule waendelee sasa kuwekeza viwanda na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, limezungumzwa kwa uchungu sana suala Liganga na Mchuchuma. Suala hili limezungumzwa kwa miaka mingi, mpaka tunajiuliza kuna tatizo gani sisi watu wa Kusini kule? Kuna tatizo gani na ni uchumi mkubwa katika Mkoa wa Njombe na Kitaifa kwa ujumla, lakini mpaka sasa hatujaona hapa nini ambacho kinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, alipokuja Waziri Mkuu tumekwenda pale Liganga mwaka huu, wale wawekezaji wametenga hela za kulipa fidia, wale wawekezaji wako tayari na Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema Kamati maalum itaundwa ya kuona je, zile fedha zilizotengwa, bilioni kumi na tatu, zinaendana na fidia ile?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimuulize Mheshimiwa Waziri, mpaka sasa wamefikia wapi juu ya kulipa fidia ya Liganga na Mchuchuma ili mwekezaji yule aweze kuendelea na shughuli ile kwa sababu fedha zipo? Ni uchumi mkubwa sisi tunaoutegemea sana katika Liganga na Mchuchuma na mwekezaji yule tunamkatisha tamaa maana sasa hatuelewi nini kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Serikali ihakikishe kwamba inalipa fidia kwa sababu fedha zipo mwekezaji anazo yeye mwenyewe na kuhakikisha wawekezaji wale wanaanza na walikuwa tayari kuanza. Bajeti iliyopita mlituambia mwaka huu wa 2016/2017 mwekezaji ilitakiwa aanze, nini kimechelewesha? Tupate majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, leo katika Wizara hii kwa kweli inafanya kazi nzuri ya kuhakikisha viwanda vinajengwa katika nchi yetu na ndio uchumi. Tukiwekeza kwenye viwanda tutapata ajira na kadhalika. Nakubaliana kabisa Mheshimiwa Mwijage anafanya kazi nzuri pamoja na watendaji wake na Naibu Waziri, lakini nirudie tena, nasema kwa uchungu kabisa, wale watu wa Makambako hivi sasa wako njiani wanakuja, kwa hiyo jioni Mheshimiwa Mwijage anao na Mheshimiwa Waziri Mkuu jioni atatakiwa akutane nao, kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema majibu nitarudi nayo mimi, sasa wanakuja. Nimwombe jioni ahakikishe anakutana na hao watu wa kutoka Makambako.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili linanipa tabu, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu nitakaposhika shilingi juu ya kulipa fidia ya watu hawa mniunge mkono, kabisa, yaani Mbunge mwenzenu napata tabu juu ya watu hawa kulipwa fidia. Kwa sababu kwenye bajeti humu ya mwaka huu hazimo sasa maana yake mpaka mwezi Juni hii zilitakiwa ziwe zimeshalipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage sijui nisemeje, wale watu wananipa tabu kwa kweli. Yaani nakosa raha juu ya kulipa fidia hizi, niiombe sana Serikali yangu. Mheshimiwa Rais alishasema fidia ilipwe sasa nini? Yamechukuliwa makaratasi yote yanayotakiwa ya wale watu, wako 274 yako kwenu Hazina na Mheshimiwa Mwijage anayo.

T A A R I F A . . .

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, unajua tungekuwa tunaelewa kwamba Waheshimiwa Wabunge wote humu ndani tunatekeleza Ilani ya CCM tusingesema hivyo. Wote hapa tunatekeleza Ilani ya CCM ndiyo tuliyopata ridhaa, ndiyo maana naiambia Serikali yangu ya CCM itekeleze Ilani ambayo tulishaiambia. Kwa hiyo wote humu tunatekeleza Ilani ya CCM.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana, nadhani ameelewa humu ndani wote tunatekeleza Ilani ya CCM, ndiyo inayosimamiwa na ndiyo maana tunaiambia Serikali sasa yale mambo ambayo iliahidi iweze kutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimalizie tu kwa kusema Mheshimiwa Mwijage na watendaji wake, wamenielewa nilichokisema, niombe sana kuhakikisha mpaka Juni, angalau wale watu tuwalipe fidia zao kama ambavyo tulikuwa tumeahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo haya nikushukuru sana, niishukuru Serikali, nimshukuru Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya. Naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Kwanza naunga mkono ushauri wa Kamati ya Kilimo na Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuru Serikali ya CCM inayoongozwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli, pamoja na Mawaziri, Waziri wa Maji, Naibu Waziri pamoja na wataalam wa Wizara hii ya Maji pamoja na Mawaziri wote wa Wizara zote kwa kazi nzuri wanazozifanya za kutekeleza Ilani ya CCM. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze kama mchumi. Imezungumziwa hapa kwamba fedha zilizotengwa kutoka mwaka jana, shilingi bilioni 900 ya 2016/2017 na sasa zimetengwa fedha pungufu utofauti na nani!

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naipongeza sana Wizara kupitia wataalam, wametenga kitu ambacho ndio uhalisia ambao fedha zitakwenda kwenye miradi. Kwa sababu fedha zilizotengwa mwaka jana hatukuzifikia na ndiyo maana wameonesha hapa tumefikia asilimia 19. Kwa hiyo, nawapongeza sana wataalam wa Wizara hii kwa maana wametenga sasa fedha ambazo zinakwenda kutekeleza uhalisia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na wenzangu ambao wamesema iongezwe tozo ya shilingi 50. Naungana nao kabisa kwamba angalau itaongeza fedha katika huu Mfuko wa Maji. Kamati ya Bajeti watakwenda kukaa kuona namna ambavyo hii tozo yashilingi 50; nadhani tutakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipate maelezo mazuri Mheshimiwa Waziri atakaposimama, katika miradi ile iliyopata fedha kutoka Serikali ya India ambapo kuna miradi 17 katika Tanzania Bara na Zanzibar ikiwemo na Makambako; watueleze kwa sababu tayari hapa baadhi ya Wabunge tumekuwa na wasiwasi kwamba fedha hizi ambazo zimekuwa zikitoka nje tumekuwa hatuzipati. Sasa naomba Mheshimiwa Waziri atakaposimama atueleze kwa kina uhakika wa kupata fedha hizi ili wananchi wangu wa Makambako wajue fedha hizi zitakwenda kutekeleza mradi ambao Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba shughuli ya maji Makambako itatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuna Mradi wa Bwawani wa Bwawa la Makambako ambao ni tofauti na mradi huu mkubwa. Mradi huu ulishatangazwa na Mamlaka ya Maji Iringa (IRUWASA) wanaosimamia. Na ilivyotangazwa suala hili liko Wizarani. Nataka nipate majibu nini sasa kinaendelea ili wananchi wa Makambako wajue mradi huu sasa umefikia hatua gani kwa sababu umetangazwa na una muda mrefu tangu watangaze, zaidi ya miezi miwili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo, niwaombe Wizara, fedha kwa mfano zilizotengwa mwaka jana mpaka sasa mtusaidie wenzetu ma-engineer walioko huko, wataalam wa maji, mpaka sasa kuna baadhi ya miradi haijatangazwa. Sijajua kuna kigugumizi gani? Mtusaidie Wizara wanaohusiana na mambo ya Mkoa kule na kadhalika ambapo fedha hizi zilizotengwa katika eneo langu zingeweza kusaidia kupata maji katika vijiji vifuatavyo; vijiji vya Mbugani, Mawande, Mtulingala, Mahongole, Usetule na Ibatu wangepata maji. Lakini vilevile Mheshimiwa Waziri nisaidie kuna mradi mkubwa ule wa Tove ambao unahudumia vijiji kadhaa, vimeishia pale Ilunda. Ilunda pale kuja kwenye kijiji cha Ikelu ni kilometa mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mradi unasimamiwa na nani? Nani ambaye anazuwia wananchi pale Ikelu wasipate maji? Naomba utakaposimama hapa Waziri uniambie kwa sababu maji pale yako mengi na kadhalika, hawapati maji pale…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niwe mtu wa kwanza kuanza kuchangia hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nachukua nafasi kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli pamoja na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu na Waheshimiwa Mawaziri wote kwa kazi nzuri wanazozifanya kuwaletea maendeleo wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la elimu. Naishukuru tena Serikali kwa namna ambavyo imeanzisha mpango wa elimu bure, hivi sasa wanafunzi wamekuwa ni wengi sana katika mashule yetu. Kuna shule kwenye Halmashauri yangu ya Mji wa Makambako; Shule ya Ikwete, Shule ya Mashujaa na Shule za Juhudi. Shule hizi ni za siku nyingi, zimechakaa sana majengo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kwa namna ya kipekee kabisa ikishirikiana na wananchi nami Mbunge wao pamoja na Waheshimiwa Madiwani, tuone namna gani tunajiimarisha kuweza kujenga shule hizi ili zifanane na shule nyingine ambazo zipo hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la pili la afya. Naipongeza sana Serikali kwa dhati kabisa kwa kazi nzuri inayofanya katika maeneo yetu kwa kutenga fedha nyingi kupeleka katika Vituo vya Afya, Zahanati na Hospitali. Kazi hiyo ni nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, katika Halmashauri ya Mji wangu wa Makambako tuna Kituo cha Afya kimoja, kinachoitwa Lyamkena. Tunaomba na sisi pia tupewe fedha kama ambavyo zimepewa Halmashauri nyingine ili nasi Kituo cha Afya hiki kiweze kufanya kazi za upasuaji na kama ambavyo vituo vingine vinafanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali kwa kutenga fedha ambazo wamenipa kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Mji wa Makambako. Naishukuru sana. Pia katika Hospitali ya Mji wa Makambako niiombe Wizara au Serikali, Kituo cha Afya kilipandishwa hadhi tangu mwaka 2013 na kuwa hospitali, lakini mgao wa dawa bado tunapata kama Kituo cha Afya wakati ni hospitali. Naiomba sana Serikali itupe mgao wa dawa kama hospitali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu ni maji. Naipongeza Serikali kwa dhati kwa namna ambavyo imenipa fedha za miradi katika Kijiji cha Ibatu, Usetule, Mtulingala, Mahongole na Mbugani - Nyamande, Kiumba na Ikelu. Hivi sasa shughuli za maji kule zinaendelea. Naipongeza sana Serikali kwa namna ambavyo inataka kumtua mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naiomba Serikali, kuna mradi mkubwa ule wa fedha za kutoka India ambazo zilitengwa kwenye bajeti. Mradi ule wa miradi 17, Tanzania Bara miradi 16 na Zanzibar mradi mmoja (1). Katika miradi hiyo na Makambako ipo na Njombe Mjini ipo na Wanging’ombe ipo. Naomba kujua, ni kitu gani kinakwamisha mradi huu usianzishwe? Kwa sababu tulipata taarifa wakati fulani, alikuja Waziri wa India pale Ikulu, alisaini mkataba huu. Tatizo ni nini? Kimekwamisha kitu gani mradi huu hauanzi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ione namna ambavyo itaanzisha mradi huu wa fedha za kutoka India ili kutatua tatizo la Mji wa Makambako katika suala hili la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu ujenzi. Alipokuja Mgombea ambaye ni Rais sasa, katika Mji wa Makambako, alituahidi kutupa kilomita sita za lami katika Mji wa Makambako. Mpaka sasa hata kilomita moja haijaanza. Kila nikiongea na Mheshimiwa Waziri, amekuwa akiniambia kwamba safari hii ilitengwa kilomita mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali angalau wangeanza kwa kilomita mbili hizi, angalau katika Mji wetu wa Makambako, ungekuwa ni mji unaopendeza kupitia barabara zake za lami. Siyo hivyo tu, naiomba pia TARURA, katika Mji wa Makambako kuna barabara ya kutoka pale Makambako kwenda Maguvani. Maguvani ni eneo la sekondari, pana korongo kubwa katikati. Naiomba Serikali itupe fedha za dharura kwa sababu hivi sasa wanafunzi wanaotoka ng’ambo kwenda katika shule hii ya Sekondari ya Maguvani wanazunguka Mjini Makambako ambako ni kilomita 10 wakati pale ni kilomita moja na nusu tu. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali ione namna ya kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la TARURA vile vile, tuna stendi ya Mji wa Makambako. Stendi ile ndiyo stendi kubwa lakini maji yote yanapotiririka yanakwenda kwenye majumba ya watu na nyumba kadhaa zimeanguka. Naiomba Serikali ituwekee makalavati ambayo yatanusuru nyumba hizi za wananchi katika stendi kuu ya Makambako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alipokuja Rais katika Mji wa Makambako alituahidi kutujengea uwanja wa mpira. Tumeshaandaa uwanja na mpaka sasa hakuna kinachoendelea. Naiomba sana Serikali kuona namna ya kutimiza ahadi hii ya Mheshimiwa Rais kwa wananchi. Kila wakati tumekuwa tukiwaambia kwamba muda bado, tunaiomba sasa Serikali ichukue jukumu la kuhakikisha uwanja huu unajengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwenye suala la umeme kwa nchi nzima na hususan katika Halmashauri yangu. Vijiji vingi sasa Mkandarasi yuko site anaendelea kuweka nguzo. Naipongeza sana Serikali kuona sasa katika vijiji vyote vya Halmashauri ya Mji wa Makambako vitapata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, katika Kijiji cha Kifumbe kwenda Kijiji cha Mtanga ni kilomita tano mpaka sita. Shughuli hii Mkandarasi anayoendelea nayo, kijiji kitakachobaki katika ukanda huo ni hicho peke yake. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali, ione namna ya kuona kijiji hicho nacho kinaunganishwa katika awamu hii inayoendelea hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ione namna ya kuanzisha mashamba kwa ajili ya mbegu mbalimbali za kilimo hasa mahindi katika ukanda wetu. Tatizo la mbegu limekuwa ni kubwa sana. Utaona wakati fulani baadhi ya watu wamekuwa wakichakachua mbegu, ni kwa sababu mbegu hizi ni chache. Kwa hiyo, naomba sana Serikali ione namna ya kuanzisha mashamba kwa ajili ya mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna Mawakala waliosambaza pembejeo. Hivi sasa ni zaidi ya miaka mitatu, hawajalipwa. Naiomba Serikali kama kuna baadhi ambao walifanya kazi nzuri katika kufuatilia na katika kuhakiki, basi walipwe. Wale ambao walichakachua wakafanya udanganyifu waambiwe kwamba ninyi hamlipwi kwa sababu mmefanya udanganyifu, lakini wale waliofanya vizuri walipwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu fidia kwa soko la Kimataifa, Makambako. Wale watu sasa imekuwa ni tatizo kubwa. Naiomba Serikali, wakati fulani wameandamana, wamejaa kwenye mafuso kwenda Dar es Salaam na wakasema watashuka pale Ikulu, kama kuuawa wauawe. Nilimwambia Mheshimiwa Waziri wa Fedha, nilimwambia, nikawasihi. Naiomba sana Serikali, chonde chonde tuone namna ya kuwalipa fidia hawa watu. Zaidi ya miaka 21 sasa hawajalipwa fidia, kwa hiyo, imekuwa ni tatizo kubwa sana. Naomba sana walipwe fidia watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana wakati nachangia suala la Mambo ya Ndani, naomba niseme kama ifuatavyo: Makambako ndiyo center. Unapozungumzia kwenda Mbeya, Makambako ndiyo center; unapozungumzia kwenda Songea, Makambako ndiyo center; unapokwenda Iringa, Makambako ndiyo center. Ni center wakati fulani baadhi ya wahalifu ndiyo wanakimbilia pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie Waheshimiwa Wabunge, hata wale waliokuwa wanafanya uhalifu kule Kibiti walipatikana baadhi ya wawili, watatu pale Makambako. Nikaenda mimi pale Polisi wakaniambia Mheshimiwa Mbunge njoo uwaone watu hao. Walikimbia kumbe wakaenda Songea. Walipoona Songea msako mkali, wakakimbilia Makambako. Kwa hiyo, naomba sana, tuone katika magari yatakayokuja ambayo Mheshimiwa Waziri jana alisema, katika mgao tuone… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Kwanza niungane na wenzangu kuipongeza Serikali inayoongozwa na Dkt. John Pombe Joseph Magufuli pamoja na Mawaziri wote pamoja na Waziri mwenye dhamana ya Wizara ya Afya na watendaji wake wote, Makatibu Wakuu na kadhalika. Kazi ambayo inafanywa na Serikali hii hakuna mfano, ni kazi nzuri sana ukienda kwenye idara na wizara mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie hii moja tu ya afya. Katika halmashauri yangu ya Mji wa Makambako tumepewa fedha shilingi bilioni moja milioni mia tano kwa ajili ya kujenga hospitali yetu ya Mji wa Makambako. Tumepewa shilingi milioni mia saba kwa ajili ya kuboresha kituo chetu cha afya katika Kata ya Lyamkena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali, naomba sana katika hospitali au kituo kilichopo Makambako pale; pale ni centre. Dawa tunazopata hazikidhi, tunahitaji tuongezewe dawa ili ziweze kuhudumia watu wetu; na ndiyo maana na mimi nimeunga mkono jitihada za Serikali zinazofanywa na nimejenga vyumba viwili vya Madaktari pale vitafunguliwa mwishoni mwa mwezi huu, vyumba viwili vya kutolea huduma vya Madaktari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wanazungumza; Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi amewahi kusema kwamba Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa aliyofanya kwa miaka miwili katika sekta mbalimbali ni sawa na miaka 10, hakuna mfano. Sasa kwa kazi hizo ambazo anazifanya; ukienda kule China Rais wa China amepewa kuwa ni Rais wa maisha kutokana na kazi anazofanya, kwa nini Magufuli asiwe Rais wa maisha kutokana na kazi anazofanya? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka miwili tu kazi ambayo amezifanya ni nzuri na kubwa. Kwa kweli lazima tumuombee kwa Mwenyezi Mungu aendelee kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako watu hapa kazi yao ni kubeza. Nilikuwa namsikia mtu mmoja akisema hizi hela ambazo zimewekwa hapa kwenye bajeti kama hazitaenda hizo hela basi nipeni mimi. Wako watu hapa wanabeza, jamani hii ni bajeti, ni mwelekeo wa bajeti, lazima tuishukuru Serikali kwa kazi inazofanya. Mnasema kama hizi hela zimewekwa tu, kama haziwezi kwenda; amesema mwenzangu mmoja kule kwa hata unapoamka unasema Mungu wangu tunakuomba na kadhalika; lakini yako mambo unamshukuru na kumwomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hebu tamka unanijua? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali kwa kweli kwa kazi nzuri ambazo zinafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nimalizie, pamoja na dakika chache hizi niiombe sana Serikali; tumejenga zahanati 10, tumeshaezeka, tumepiga lipu, tuko hatua za mwisho. Tuiombe Serikali mtutengee fedha kwa ajili ya kumalizia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, mimi pamoja na Wabunge wenzangu wa Mkoa wa Njombe, tunaipongeza Serikali kwa kutujengea Hospitali ya Mkoa wa Njombe. Jengo la OPD limeisha, ombi langu kuwa fedha zilizotengwa hapa tuone namna ya kumalizia hospitali ile ili ianze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na Mungu akubariki sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anaozifanya pamoja na Mawaziri wote; Waziri Mkuu, Waziri mwenye dhamana na Naibu Mawaziri wa Wizara hii ambayo tunachangia pamoja na Makatibu wake na wote wanaomsaidia katika Wizara hii. Kazi zinazofanyika tunaziona, ni nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende sasa kwenye Jimbo langu la Halmashauri ya Mji wa Makambako. Pale Makambako kuna eneo fulani panaitwa Idofi ambapo Wizara walikuwa wamesema tuandae kwa ajili ya kujenga One Stop Centre na eneo hili kazi iliyofanyika kuwaomba wananchi wale ni kazi kubwa, ngumu na ambayo mpaka sasa hatuelewi nini kinachoendelea na kwa sababu bado hawajalipwa fidia na kwenye kitabu nilikuwa naangalia sioni mahali ambapo panaonyesha utayari wa kujenga one stop center kwa ajili ya manufaa ya watu wa Makambako, ombi langu niombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapo atueleze One Stop Center ipo au haipo. Na kwa sababu pana msongamano sana wa magari na nini pale, wenyewe mnaona mnapokwenda Songea, Mbeya, pana msongamano mkubwa sana wa jam ya magari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili; niishukuru tena Serikali kwa namna ambavyo imetenga bajeti kwa ajili ya kutengeneza kilometa sita za Mji wa Makambako ambazo Mheshimiwa Rais aliahidi na sasa naziona hapa, nawapongeza sana na shughuli hiyo nimeiona pale sasa imeshaanza kwa mita 150, najua kwamba sasa wakati mkandarasi anaendelea na bajeti hii itakuwa imeshafika muda wake mtaendelea kuikamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna barabara ambayo ni ya TANROADS, unapokwenda Songea road pana Kijiji kinaitwa Ilunda, kutoka Ilunda kwenda Igongolo pana kilometa tisa ambazo ni za TANROADS, ukiendelea mbele barabara hii mbele inaendelea inakwenda Ilengititu, inakwenda Kifumbe, Mahongole inakuja kutokea Makambako na utaona sasa barabara hii kwa kilometa tisa ambazo zimetengenezwa pale barabara mbele inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu ni kwamba barabara hii sasa iingizwe kwa TANROADS ili kusudi kwa mzunguko huu pale ni kilometa 19, ili mzunguko wa barabara kwenda kutokea Makambako uweze kuwa mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima niipongeze tena Serikali kwa barabara ya kutoka Nyigu kwenda Igawa ambayo inapita pale kwangu Makambako, kazi inayofanyika ni nzuri sana. Ombi langu ni kwamba zile barabara za pembeni na zenyewe, naona wanaendelea, basi nina imani kwamba mtakamilisha vizuri kama ambavyo iko ile waliyokamilisha pale Mafinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze tena barabara ya kutoka Makambako kwenda Songea ambayo nimeiona iko kwenye bajeti. Ombi langu kwa Wizara, barabara hii kwenda Songea ukitoka Makambako kwenda Njombe vichepu vya basi kipo kimoja tu kiko pale Mtwango, utaona hakuna mahali ambako mabasi yanaweza kusimama na nyumba zimejaa kutoka Makambako mpaka Njombe. Ombi, muone namna ya kupanua mabega ili kuwe na vituo vya basi kwa ajili ya barabara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye mawasiliano, katika mawasiliano kutoka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba dakika moja tu, kuna jambo muhimu. Nije kwenye suala ambalo Rais analifanya, Mheshimiwa Rais wetu amekaa hapa ndani kwa miaka 20 akisikiliza hoja mbalimbali ambazo zilikuwa zinasemwa pande zote mbili. Hoja hizo sasa ndiyo zinatekelezwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri waliyoifanya kwa kuwapa fidia wananchi wangu wa Jimbo la Makambako. Nawashukuru sana, kwa dhati kabisa kwa sakafu ya moyo wangu, nawashukuru sana, wamefanya kazi nzuri. Kwa sababu fedha hizi wamezidai kwa muda mrefu, lakini kupitia ahadi ya Mheshimiwa Rais imetekelezwa. Narudia tena kuwashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaposhukuru, kuna ombi tena kuhusu fidia nyingine. Pale Makambako kupitia Wizara ya Ujenzi, wana eneo ambalo waliomba, tuwaombe wananchi kwa ajili ya kujenga One Stop Centre katika Kijiji cha Idofili, kilometa tano tu kuingia Mjini Makambako ukitokea barabara ya Iringa. Katika eneo hilo, vile vile kunatakiwa kulipwa fidia ili waanze kujenga One Stop Centre. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri katika hitimisho lake, basi aseme neno ili roho za wananchi wangu wa Jimbo la Makambako waweze kupona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, tuna Liganga na Mchuchuma. Imezungumzwa kwa muda mrefu sana kuhusu uchumi wa Liganga na Mchuchuma. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Fedha, atuambie ni nini kinachokwamisha Liganga na Mchuchuma isitekelezwe au isianze? Kwa hiyo kwenye hitimisho pia nitaomba nipate majibu, tatizo ni kitu gani ambacho kinafanya isianze? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine tumejenga zahanati nyingi sana katika nchi yetu ambayo magofu haya ni mengi ikiwepo Jimbo la Makambako. Makambako tuna zahanati ya vijiji zaidi ya 13 ambazo wananchi, Waheshimiwa Madiwani, Serikali, Mfuko wa Jimbo pamoja na mimi Mbunge wao tumejenga zahanati hizi. Ombi langu kwa Wizara ya Fedha, tuone sasa ni namna gani kwa nchi nzima na kupitia hata Halmashauri yangu ya Makambako tuzimalize zahanati hizi ili zianze kufanya kazi kusogeza huduma kwa wananchi wetu na hasa akinamama na watoto.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine napenda sana Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha, nipate majibu hasa ya miradi ya maji 17 nchini ikiwepo na Makambako kwa fedha za kutoka Serikali ya India kwa mkopo nafuu. Maana mpaka sasa hatuelewi kazi hii inaanza lini. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri pia katika miradi hii 17, mmojawapo upo Njombe, Makambako, Wanging’ombe na mahali pengine Zanzibar kule kuna mradi mmoja nadhani. Basi ni vizuri Mheshimiwa Waziri atuambie ni lini miradi hii itaanza ili wananchi waweze kupata huduma hii ya maji kama ilivyokusudiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, katika Wizara mbalimbali ambazo tumekuwa tukichangia hapa ndani, Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema, nami naomba niseme Mheshimiwa Waziri. Namwomba Waziri wa Fedha, fedha hizi za miradi mbalimbali basi ziende kwa wakati ili shughuli zilizopangwa kule kwenye Halmashauri yetu ziweze kwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Mheshimiwa Waziri, kupanga ni kuchagua. Kuna watu walizungumzia habari ya kununua ndege, habari ya reli, habari ya huo umeme kwamba huo umeme wa kutoka Bonde la Rufiji hauna manufaa na reli haina manufaa. Niseme kwamba Bunge lililopita la mwaka 2010 - 2015, Waheshimiwa Wabunge walisema hapa, ni nchi ya ajabu hii kutokuwa na ndege zake yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo Serikali imetii kupitia Mheshimiwa Rais wetu, maana alikuwepo Bungeni hapa wakati ule akiwa Waziri, leo ametii, amenunua ndege katika nchi yetu, tunasema kwa nini amenunua ndege, hazina manufaa. Tukiwa hapa Bunge la mwaka 2010/2015 tulizungumzia hapa, ni nchi gani haina reli? Reli hii ya kati ni reli ambayo imepitwa na wakati, tunataka standard gauge. Mheshimiwa Rais ametii, amekubali, sasa ametafuta fedha tunajenga reli ya standard gauge. Kupanga ni kuchagua ndugu zangu, ni lazima tusiwe vigeugeu, tuiunge mkono Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulizungumzia hapa kwamba wawekezaji wanashindwa kuja ni kwa sababu umeme hautoshi. Leo ufumbuzi umeme kutoka Bonde la Rufiji, tunasema ule mradi haufai. Sasa tunajikatisha tamaa wenyewe kwa wawekezaji wanaokuja kwamba kumbe umeme kule haupo. Tuunge mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano juu ya mipango mizuri ambayo ipo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mpango na Wizara yake na Watendaji wake, achape kazi asonge mbele. Mipango ni mizuri sana. Kwa hiyo, sisi tuko nyuma yako, tunamuunga mkono kupitia bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, wenzangu wamesema hapa, Mheshimiwa Waziri amekuwa muwazi, ameeleza kila jambo; hili liko hapa, hili bado hivi, hili liko hivi. Tunamuunga mkono, achape kazi, asonge mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niungane na wenzangu kujadili Mpango huu wa mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii ya kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli pamoja na Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa, pamoja na Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kazi nzuri ambayo leo tunaijadili hapa ya Dkt. Mpango, kwa kupitisha bajeti ile ambayo tulikuwa tunakaa hapa na ndio sasa tunayaona yaliyokuwa yanafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mpango tunakupongeza sana na timu yako na wataalam wako na Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo ipo mbele yetu, kwa kweli lazima tuwe wakweli, nianze na Wizara ya Afya, Mheshimiwa Mpango imezungumzwa hapa kuna baadhi ya watu wanasema bajeti iliyoongezeka zaidi ya bilioni mia mbili na kitu bado hawaoni maana yake, mimi nimebaki nashangaa Waheshimiwa Wabunge. Hivi bajeti ile si baadhi ya vituo, zahanati na vituo vya afya ambavyo vimejengwa si lazima fedha ziongezeke? Kazi nzuri imefanywa sana na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti kazi nzuri iliyofanywa na Serikali ikiwepo kwenye jimbo langu vituo afya viwili vimeongezeka na hospitali ya Wilaya ya Halmshauri, lazima tuipongeze Serikali kwa kazi nzuri ambayo inafanywa hivi sasa kituo cha afya kwenye jimbo langu mwezi wa pili kinafunguliwa kwa fedha ambazo Serikali ya Awamu ya Tano kama walivyosema wenzangu vituo zaidi ya 300 na kila Jimbo nadhani vituo hivyo vipo. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali hata mwenzangu jirani ananiambia hata Tarime vipo, eeh kwa hiyo lazima tuipongeze sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile tukija kwenye upande wa maji, mwenye macho haambiwi tizama maji katika nchi nzima asilimia kubwa imepungua hata kwenye jimbo langu tu suala la maji ipo miradi inaendelea pale iko miradi mingi katika jimbo langu, ni fedha tu kwa hiyo Mheshimiwa Mpango tunakupongeza. Ipo miradi ile 26 ya maji katika nchi, katika miradi 26 mradi mmoja upo kwenye jimbo langu katika mpango huu wa wewe Mheshimiwa Mpango. Sasa tunaipongeza sasa Serikali ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija miundo mbinu ya barabara za kuunganisha mikoa kwa mikoa, leo mtu anatoka kule Mbinga kwa Mheshimiwa Mapuda, anatoka Mbinga asubuhi ikifika usiku anakuwa Mwanza, barabara zimetengezwa ni fedha hizi za Awamu ya Tano. Kwa hiyo tunaipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija barabara pale kwangu pia kwenye jimbo langu barabara za lami zinatengenezwa, ukitoka pale iko barabara ambayo barabara kuu ya kutoka Dar es Salaam - Zambia sasa hivi kwenye jimbo langu pale Makambako barabara na viunga vyake vinapendeza sana, kwa hiyo tunaipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumzia hapa reli wenzetu wa kanda ya ziwa wamekuwa wakipata taabu sana juu ya reli hii ya kati, Serikali imechukua jukumu ya kuishughulikia reli hii, watu wanasema aaa mpango sio reli; kupanga ni kuchangua. Tunakupongeza sana Mheshimiwa Mpango kwa namna ambavyo umeelezea hapa kwamba reli hii lazima inakamilika songa mbele kama alivyosema mwenzangu Mheshimiwa Ndassa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukija upande wa ndege, nimewahi kusema hapa Bunge la mwaka 2013 hapa na baadhi watu walikuwa wanazungumizia hapa duniani kokote kule hamuwezi kuwa mkawa hamna ndege za nchini kwenu, Rais amechukua jukumu la kununua ndege katika nchi yetu, tunaipondeza sana kwa taarifa hii ambayo kuna ndege zingine zinakuja mwakani mwezi Novemba, tunakupongeza Dkt. Mpango na Serikali ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi nzuri ambapo ndege hizi zitapunguza kero mbalimbali ambazo watu walikuwa wanapata tabu kusafiri lakini zitaongeza utalii wa ndani, Mheshimiwa Mpango songa mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipofanya ziara kwenye Jimbo langu mikutano 65 nimefanya kila siku nilifanya mikutano mitatu hakuna mwananchi hata mmoja aliporuhusiwa kuuliza maswali aliyezungumzia Katiba hayupo hata mmoja hayupo! Hata mmoja hayupo, watu walikuwa wanaauliza habari ya maji, barabara, pembejeo na kadhalika hakuna. Sasa leo tuanze kupoteza fedha kwa ajili ya Katiba, niombe sana Serikali na Rais na Waziri Mkuu upo hapa msijadili habari Katiba wananchi sio tatizo Katiba. Tatizo ni maendeleo katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa kazi iliyofanya Serikali ya Awamu ya Tano, tumuombe Mheshimiwa Spika na Wabunge wote baada ya kumaliza Bunge hili sijajua linaisha lini tufanye party ndogo ya kuipongea Serikali kwa kazi nzuri iliyofanywa, kwa hiyo, nikuombe Mwenyekiti jambo hili lipewe kipaumbele tufanye party ndogo ya kuipongeza Serikali kwa namna ambavyo inafanya kazi na leo narudia, kwa kazi iliyofanywa kwa miaka mitatu unadhani ni kazi ya miaka 20 huo ndio ukweli. (Makofi)

Sasa narudia kwa maneno haya niliwahi kusema Bungeni hapa, Rais wa China kwa kazi nzuri amekuwa akifanya na Marais wengine nchi mbalimbali wenzetu kule walisema awe Rais wa maisha. Narudia Rais huyu awe Rais wa maisha kutokana na kazi nzuri anayoifanya, lazima tuwe wa kweli, lazima tuwe wa kweli hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo naunga mkono hoja, ya Mpango wa Dkt. Mpango kwa kazi nzuri, songa mbele na nakushuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nami niungane na wenzangu kukushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze na jambo ambalo limezungumzwa sana jana leo na tangu huko nyuma kuhusu udhaifu wa sisi Wabunge.

Mheshimiwa Spika, hawa wenzetu upande wa pili, katika bajeti ambazo tumekuwa tukipitisha hapa hawajawahi kusema ‘ndiyo’ hata mara moja. Kwa maana hiyo, wanataka kutuchelewesha kwa kazi nzuri zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. Kazi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano pamoja na Waziri Mkuu na Mawaziri pamoja na wewe mwenyewe Spika ambaye unatusimamia kuisimamia Serikali, ni kazi nzuri sana. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali kwa namna ambavyo Waziri Mkuu amewakilisha hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo, nianze kwa kuishukuru Serikali kwa namna ambavyo kwenye Jimbo langu la Makambaku, kwa namna ambavyo wananchi wangu wamekuwa wakilia juu ya kulipwa fidia kwa Soko la Kimataifa zaidi ya miaka 18; mwaka 2018 kupitia Ofisi hii inayosimamiwa na Mipango na Waziri, amelipa fidia zaidi ya shilingi bilioni tatu na kitu. Natoa shukrani sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu ni kwamba kuna baadhi ya watu kumi na kitu hawakuwepo wakati wa uhakiki, naomba sana watu hawa walipojitokeza watu wa uhakiki walikuwa wameondoka. Kwa hiyo, naomba waweze kuhakikiwa ili nao waingie kwenye kulipwa fidia.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili naiomba Serikali, kuna eneo pale pale Idofyu kuna mpango wa kujenga one stop center, sasa napo tunahitaji wananchi wale kulipwa fidia. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali, kwenye mpango huu iweze kuwalipa fidia wananchi wangu wa Makambaku.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, naishukuru Serikali kwa suala la umeme awamu ya tatu. Kwenye Jimbo langu natoa shukrani kubwa sana, najua na Watanzania wenzangu, Waheshimiwa Wabunge wenzangu ni hivyo hivyo. Napongeza sana kwa namna ambavyo wananchi, wameweza kupata umeme katika maeneo yote ya Jimbo langu la Makambaku.

Mheshimiwa Spika, ombi kwa Serikali, kuna kijiji kinaitwa Mtanga ambako umeme umefika kule Kifumbe, pale ni kilometa tano, kimebaki peke yake; naiomba Serikali iwapatie umeme ili nao waweze kufaidi kama ambavyo wenzao wanafaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile niishukuru pia Serikali kwa namna ambavyo imeweza kutupa fedha katika vijiji kadhaa kwa ajili ya suala la maji. Kwa kweli naishukuru sana. Ombi, tunataka kujua, fedha hizi za mkopo nafuu kutoka India ni lini mradi huu utaanza ili wananchi wa Makambaku waweze kufaidika na mradi huu mkubwa ambao utatatua changamoto kubwa kabisa ya maji iliyopo katika mji wetu wa Makambaku na Kijiji cha Ikelu?

Mheshimiwa Spika, mimi nimekuwa Diwani kwa miaka 10. Mpango wa afya kwa namna ambavyo Serikali imetoa fedha nyingi kwenye Vituo vya Afya, nami ni mmojawapo nimepata. Kwa hiyo, naishukuru sana Serikali kwa dhati kabisa. Vile vile tumepata fedha kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Rufaa ya Halmashauri ya Mji wetu wa Makambaku, shilingi 1,500,000,000/= na hivi tunakwenda vizuri, naishukuru sana Serikali kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi, tuna Kituo cha Afya ambacho tulikuwa tunakiita Hospitali ya Mji wa Makambaku, tupate X-Ray kwa ajili ya huduma mbalimbali katika mji wetu wa Makambaku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wa TARURA tunakwenda vizuri. Tunaiomba Serikali iongezee fedha upande wa TARURA ili barabara zinazounganisha baadhi ya kijiji na kijiji ziweze kupitika vizuri. Naomba Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana anayehusika; Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa Rais mgombea wakati ule 2015 tuliahidiwa kilomita sita za lami katika Mji wa Makambaku. Mpaka sasa zimetengenezwa mita 150. Ombi langu ni kwamba barabara hii ya kilomita sita iweze kutengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kilimo. Amezungumza Mheshimiwa Vuai Nahodha hapa; suala la kilimo ni asilimia kubwa sana ya wakulima wetu na mbolea ambazo wanazipata ziko bei juu, haziwiani na mauzo ya mazao yanayozalishwa. Nini kifanyike?

Tunaiomba Serikali ione namna ya kusimamia bei ya pembejeo ili ziweze kupungua ziendane na uzalishaji wa kilimo, lakini vilevile tunaiomba Serikali ilete wawekezaji kwa ajili ya kujenga Kiwanda cha Mbolea ili mbolea hii iweze kuwa bei chini na izalishwe nchini kwetu hapa hapa.

MBUNGE FULANI: Kweli.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, jambo lingine, tuna maboma ya Zahanati kwa nchi nzima. Kwangu peke yake kuna maboma ya zahanati zaidi ya 13 katika vijiji. Tunaiomba Serikali, katika mwaka huu wa fedha wa 2019/ 2020 angalau ione namna ya kutoa fedha nyingi ili maboma haya yaweze kupungua. Kila Jimbo angalau maboma matano au mangapi, tukifika 2020/2021 tunaweka tena bajeti maboma haya tutakuwa tumeyamaliza. Kwa hiyo, ombi langu ni kwamba Serikali iongeze fedha kwenye maboma haya.

Mheshimiwa Spika, nilisema hapa kipindi kilichopita na leo naomba nirudie; mwenzangu amesema kwamba kiongozi wetu, Rais wetu ana maono makubwa sana, wote hapa tunakubaliana. Mipango hii mizuri iliyowekwa, nilisema hapa kwamba huyu anatakiwa aombewe awe Rais wa kudumu kutokana na mipango aliyoifanya. Sasa kama siyo hivyo, basi ili mipango hii iweze kukamilika vizuri, tuombe angalau aongezewe kipindi kimoja mpaka 2030 ili mipango yake aliyoipanga iweze kukamilika vizuri. Kama ni hivyo, mimi na Waheshimiwa Wabunge wenzangu, 2021 tutatembea nchi nzima, mimi nitakuwa wa kwanza kuwaambia Watanzania tumwombee aongezewe kipindi kingine ili akamilishe mipango na ndoto zake nzuri za maendeleo kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, wewe mwenyewe ni shahidi, hata kwenye Jimbo lako unaona namna ambavyo shughuli mbalimbali zinavyofanyika ikiwepo barabara, Vituo vya Afya, na kadhalika. Kwa hiyo, tunaiomba sana Serikali na hasa Waheshimiwa Wabunge, tutakapofika 2021 tuanze kutembea kuwaambia Watanzania, kwamba tumwongezee kipindi kingine ili ndoto zake ziweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzetu hawa ambao sasa wametoka humu ndani, watakuja tena hapa, watapinga hii bajeti ambayo tunaijadili hapa, lakini kwenye Majimbo yao wanahitaji huduma mbalimbali. Kwa sababu Rais wetu alisema maendeleo hayana chama, basi wananchi wapelekewe maendeleo, lakini isingekuwa hivyo, hawa walitakiwa walambwe na viboko kabisa. Kwa sababu wamekuja hapa kuwakilisha kwenye Majimbo yao… (Kicheko)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Sanga.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweza kuchangia. Kwanza naunga mkono hoja kwa kazi nzuri inayofanywa na Jeshi la Polisi ikisimamiwa na Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wanafanya kazi nzuri sana ya kutulinda sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana nilikuwa nasikiliza wachangiaji wenzangu hasa upande fulani, hebu fikiria Jeshi la Polisi na Mahakama visiwepo angalau kwa siku moja nini kitatokea? Ni lazima tumpongeze Waziri kwa kazi nzuri ambayo anafanya kupitia Jeshi la Polisi la kutulinda sisi na mali zetu na nchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Njombe tulipata tatizo la mauaji ya watoto. Jeshi la Polisi lilifanya kazi kubwa ya kuwakamata wahusika, hivi sasa wanajibu tuhuma walizozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nizungumzie kwenye Jimbo la Makambaku, mwaka 2016/2017 kulikuwa na mauaji vijana wengi walikuwa wananyang’anywa bodaboda zao na wanauwawa. Jeshi la Polisi limeweza kuwakamata wote waliokuwa wanafanya vitendo hivyo. Nampongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama - Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya - Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama, RPC na OCD na wapelelezi wake wa Jimbo la Kiwilaya la Kipolisi pale Makambaku. Wamefanya kazi nzuri sana, walikamata mpaka magaidi pale Makambaku, wale ambao walikuwa wanafanya mauaji kule Kibiti wamekamatwa pale na Jeshi hili hili la Polisi. Kwa hiyo, ni lazima tulipongeze sana kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili niwapongeze kwa kujenga nyumba za askari wetu kwa nchi nzima na hususan kwenye Mji wetu wa Makambaku. Tangu tupate uhuru hatujawahi kupata nyumba za Jeshi la Polisi, safari hii tumejengewa nyumba na wanaendelea kujenga nyumba nzuri za kukaa Askari wetu. Hata mimi Mbunge wao nimeweza kuchangia kwa asilimia kubwa kufanikisha nyumba zile ambazo Serikali ya Magufuli imetupa fedha. Nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo mnaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Makambaku ndiyo njia panda ya kwenda Songea, Mbeya, Iringa, tunaomba utupe gari ili Askari hawa waweze kufanikisha shughuli zao za kidoria kwenye Mji wetu wa Makambaku. Tunaomba sana tupate gari ambalo litasaidia kufanikisha shughuli za kiusalama katika Mji wetu wa Makambaku.

Mheshimiwa Spika, vilevile gereza liko Wilayani Njombe, kupitia Wizara hii ya Mambo ya Ndani tunaomba waone umuhimu wa kujenga gereza katika Halmashauri yetu ya Mji wa Makambaku. Sisi wa Makambaku tutawatafutia eneo la kujenga gereza kwa ajili ya wahalifu ambapo kwenda Njombe ni mbali. Kwa hiyo, eneo lipo, nikuombe sana Waziri mwenye dhamana uone namna ya kutenga fedha kwa kipindi kinachokuja ili kujenga gereza katika Mji wetu wa Makambaku.

Mheshimiwa Spika, nizungumze jambo la mwisho, pamoja na kazi nzuri si vizuri kuwataja hawa Askari lakini kupitia Bunge lako naomba niwataje kwa sababu ya kazi nzuri wanayofanya, akiwepo OCD wa Mji wa Makambaku, Mkuu wa Upelelezi pamoja na timu yake ya askari kadhaa wanaofanya kazi nzuri ambapo waliweza kufanikisha kukamata silaha mbalimbali katika mji wetu. Naomba muone namna ya kuwapandisha madaraja hawa askari kwa namna ambavyo wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wapo askari kadhaa ambao labda wakati fulani wanaweza kuwa si wazuri …

SPIKA: Mheshimiwa Sanga, unawapongeza askari wako wa Makambaku lakini hapa Dodoma Wabunge wote mnakaa kwa amani kabisa, salama kabisa lakini RPC wa Dodoma hamumpongezi, hii inakuwaje? (Kicheko/Makofi)

Eendelea Mheshimiwa Sanga.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, ni kweli na ndiyo nilikuwa nakuja huko kutokana na kazi nzuri wanazozifanya na hata sisi Wabunge hapa, sisi kule Iringa kuna msemo wanasema ‘tukikala kilega’, tukilegea ni kwa sababu ya usalama wa hawa wanaotulinda. Kwa hiyo na Dodoma hapa tunalindwa, tunakaa majumbani salama huko tunakokaa hakuna bughudha mitaani, tunatembea mpaka usiku wa manane ni kwa sababu ya Jeshi la Polisi. Kwa hiyo, tunawapongeza sana kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho baada ya maelezo haya, Mheshimiwa Waziri na timu yako kaza buti, endelea kuchapa kazi, askari mmoja anayeharibu si jeshi zima bovu. Kwa hiyo, hawa askari ambao wanataka kulichafua Jeshi la Polisi kupitia Kamanda wako Siro muendelee kuwadhibiti ili warudi kwenye mstari vinginevyo kazi ni nzuri na mnadhibiti vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hili suala la mikutano ambalo wenzangu wamelizungumzia hapa, kwenye mikutano watu walikuwa wanafanya kazi ya kuja kutukana si kufanya shughuli za maendeleo. Sasa hivi mikutano tunafanya kila watu kwenye maeneo yao, shughuli zinakwenda vizuri, Waziri kaza kamba. Nikutakie kila la kheri katika shughuli hizi ambazo ziko mbele yetu, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuishukuru Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Magufuli pamoja na wanaomsaidia kazi, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu yuko hapa ambaye kila wakati tunamweleza matatizo ya maeneo yetu na Mawaziri wote wanaotusaidia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nimshukuru Waziri, Mheshimiwa Ummy pamoja na Naibu Waziri wake na Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara ya Afya pamoja na TAMISEMI kwa maboresho waliyofanya ndani ya sekta ya afya. Wanafanya kazi nzuri nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na Jimbo langu la Makambako, nilipewa shilingi milioni 400 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Lyamkena, shughuli ya ujenzi imeshakamilika tangu Desemba, 2018. Tunaomba sasa tupatiwe vifaa tiba na waganga ili kituo kile kiweze kuanza kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili, tunaomba kituo mama ambacho kilikuwa kama ni hospitali ya mji wa Makambako ambacho ni Kituo cha Afya cha Makambako ambacho kinafanya kazi nzuri lakini tatizo kubwa ni ukosefu wa X-ray na Utra Sound. Mheshimiwa Rais alivyokuja tulimueleza matatizo yetu na nashukuru aliwaagiza watendaji ikiwemo Wizara ya Afya na TAMISEMI na bahati nzuri nilipokutana na Waziri wa Afya ambaye ni Mheshimiwa Ummy Mwalimu nilikueleza juu ya jambo hili na uliniahidi kwamba utanipa X-ray. Nakushukuru kwa dhati kabisa kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Makambako. Vilevile niombe sasa atakapotupa X-ray usisahau muwasiliane na wenzako wa TAMISEMI angalau tupate Utra Sound ili vifaa tiba hivi viweze kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaiomba Serikali angalau tupate fedha za kujenga wodi ya akina baba. Mlitupa fedha za kujengea wodi ya akina mama na watoto imeshakamilika na inafanya kazi katika Kituo hiki cha Afya Makambako bado wodi ya akina baba.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba tupate wodi ya akina baba kwa sababu jengo lililopo ambalo lilijengwa kwa ajili ya kuweka vifaa tiba vya X-ray na Utra Sound ndiyo vyumba kadhaa vimegawiwa vinafanya kazi kama wodi. Kwa hiyo, tunaomba tupate fedha kwa ajili ya kujenga wodi ya akina baba.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru Serikali kwa kutupa fedha za kujenga hospitali ya halmashauri yetu shilingi bilioni moja na milioni mia tano. Kwa dhati nakushukuru sana kwamba sasa tunakwenda kupata ukombozi wa tiba kwa wananchi wetu wa Makambako.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna zahanati nyingi ambazo tumezijenga katika halmashauri yetu. Halmashauri yetu kwa kushirikiana na wananchi, mimi Mbunge, Waheshimiwa Madiwani na wadau wengine zimejengwa zahanati zaidi ya 13. Tulitegemea katika bajeti hii ambayo tunaendelea nayo angalau tungepata fedha kiasi ili zahanati kadha kwa mwaka wa fedha wa 2019/2020 ziweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumefikia mahali pazuri, zimeshapigwa lipu na kadhalika. Zimeshakamilika vimebaki vitu vidogo tu. Tumeshaanza kujenga nyumba za waganga katika zahanati hizo. Naomba Serikali ione umuhimu wa kutupatia fedha mwaka huu wa 2019/2020 ili baadhi ya zahanati hizi ziweze kukamilika. Hata hivyo, naishukuru Serikali kwa kuongeza fedha kwa ajili ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, nimwombe Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Kituo cha Afya mama cha Makambako kipo katika center kubwa ya Makambako, kwenda Njombe, Mbeya, Iringa na sehemu nyingine, mtuongezee dawa kwa sababu tunapata kwa kiwango kidogo sana wakati kituo hiki kilikuwa kama hospitali kabla ya kutupa fedha za kujenga hospitali. Nikuombe sana uone namna ya kutuongezea dawa ili kukidhi kuwahudumia wananchi wa Makambako.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Kwanza nianze sana kwa kuishukuru serikali ya awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. Magufuli kwa kazi nzuri inayofanya juu ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nimshukuru Waziri Mpango na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wizara kwa ujumla kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Nichukulie tu kwa mfano; kazi ambayo Mpango unafanya nichukulie tu kwenye Jimbo moja tu la Makambako acha nchi nzima ambako kazi inafanyika kubwa; mmeweza kutupa fedha nyingi ambazo hivi sasa wakandarasi wako site wanafanya shughuli za kusogeza huduma ya maji kwa Wananchi Ikelu, Ibatu, Nyamande, Mtulingala shughuli hizo zinaendelea vizuri, nakupongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mmetupa fedha ambazo tunajenga hospitali pale ya Halmashauri ya Mji wa Makambako. Mmetupa fedha, shilingi bilioni 1,500, juzi mmetuongezea tena shilingi milioni 500. Kwa hiyo, hospitali ile inakwenda vizuri. Pia mmetupa fedha tumejenga Kituo cha Afya pale Lyamkena. Kwa hiyo, napongeza sana na kazi mbalimbali ambazo zinaendelea kufanyika katika Halmashauri yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana ukienda kwenye suala hili la uchaguzi, kwanini watu wamejitoa, wanasema Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Serikali za Mitaa amezungumzia kwamba watu wasijitokeze kwenye ofisi. Siyo kweli. Nizungumzie tu kwenye Jimbo langu; kuna Kata 12. Kata saba hakuna mtu aliyejitokeza hata mmoja. Kwa hiyo, hata kabla hawajasema hili, tulishinda tayari Kata saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa wameona mwelekeo wa nchi nzima. Hilo ni Jimbo moja. Muelekeo wa nchi nzima, wameshaona tayari ushindi haupo. Kwa hiyo, wakaona ni vizuri watangaze kwamba wanajitoa, hakuna jambo kama hiyo.

MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ehe, Mheshimiwa Sanga, hebu subiri.

T A A R I F A

MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nataka kumpatia taarifa mzungumzaji kwamba kwenye Kata zake 12 hawakujitokeza wagombea. Siyo kweli. Katika Kata zote walijitokeza Wagombea wa Chama cha CHADEMA. (Makofi)


MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Sanga, unaikubali Taarifa au unaikataa?

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua huyu ni dada yangu sasa…

MWENYEKITI: Unaikubali au unaikataa?

MHE. DEO K. SANGA: Naikataa, siyo kweli. Siyo kweli! Nitampa tu mfano. Pale Ngamanga ambako palikuwa panaongozwa na CHADEMA hawakujitokeza kwa sababu tumejenga zahanati na wao wamekiri na Mwenyekiti yule ameacha. Kwa hiyo, napongeza sana kwa kazi ambazo zinafanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kazi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano na ndiyo maana nilisema wakati ule, kwa nini Rais huyu asiwe wa maisha? Narudia tena, sasa ili mipango ikamilike kwa shughuli ambazo zimeanza za reli, ndege na kadhalika, ni vizuri muda utakapofika 2025 aongezewe hata miaka mitano ili miradi iweze kukamilika vizuri.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Bungara.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Eeeh!

MWENYEKITI: Haya.

T A A R I F A

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa Taarifa kwamba naunga mkono kwamba Katiba ibadilishwe azidishiwe muda, pia na vyama vya upinzani navyo vifutwe…

MWENYEKITI: Mheshimiwa hebu kaa chini. Kaa chini! Mheshimiwa nitakutoa nje sasa hivi, kaa chini. Mheshimiwa Sanga, endelea.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Vyama hivyo vitajifuta vyenyewe kwa sababu hawaelewi wanakwenda mbele au wanarudi nyuma. Vitajifuta vyenyewe. (Makofi/Kigelegele/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Mheshimiwa Dkt. Mpango, kwa sababu sasa tumenunua ndege zaidi ya saba na tunataka angalau sasa viwanja vyote katika mikoa yetu viweze kuruhusu ndege kutua; kiwanja chetu cha Njombe ambacho hivi sasa mlituambia kwamba kiko kwenye mpango wa kutengeneza ili ndege zetu hizi ziweze kutua. Naomba tukamilishe kiwanja kile cha Njombe ili Wana-Njombe nao waweze kusafiri kwa ndege zao ambazo zimenunuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo liko kwenye mpango ni juu ya Liganga na Mchuchuma. Liganga na Mchuchuma ikianzishwa na ikakamilika, uchumi wa Mkoa wa Njombe na uchumi wa Taifa utaongezeka kwa asilimia kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kilimo, sisi tunaotoka Kusini tunategemea sana pembejeo aina ya mbolea ya DAPO na Urea, ndizo tunazozitumia sana katika mazao yetu; na mbolea hizi ziko katika bei ya juu. Pamoja na kwamba kuna bei elekezi, tunaomba tuwe na mpango shawishi kwa wawekezaji waweze kujenga viwanda vya mbolea katika nchi yetu, angalau vitapunguza bei za mbolea na kuwa chini hasa mbolea ya DAPO na Urea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumzia juu ya kukamilishwa kwa maboma, nami naunga mkono. Tuna maboma ambayo yamejengwa na wananchi, Waheshimiwa Madiwani na Waheshimiwa Wabunge, likiwepo Jimbo la Makambako. Tumejenga maboma mengi; tuone namna ya kutenga fedha kukamilisha maboma haya, mengine yameshaezekwa, yanasubiri tu kupigwa ripu na kukamilisha na kadhalika ili maboma haya yaweze kukamilika kwa muda muafaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tuna miradi mikubwa, mmojawapo ukiwa wa maji, ule wa mkopo nafuu wa fedha kutoka Serikali ya India ambao utakamilisha miji karibu 28. Katika miji hiyo 28 na Njombe, Wanging’ombe, pamoja na Makambako ipo; tunaomba miradi hii, wananchi wanaisubiri kwa hamu sana ili kuweza kutatua tatizo la maji katika Mji wetu wa Makambako na mahali pengine ambako miradi hii itapitiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la ujumla ambalo nilitaka niseme, hili nalirudia tena; Mheshimiwa Dkt. Mpango, katika mipango ambayo umekuwa ukiipanga; ya miaka mitano na huu ambao tunaujadili hapa sasa, endelea, songa mbele. Kazi yako ni nzuri, unakwenda vizuri, Watanzania wanakutegemea. Wanategemea sana kwa mipango hii ambayo tunaijadili hapa. Mungu akubariki na akuongoze na amlinde Rais wetu ili kusudi tuweze kukamilisha miradi hii. Mawaziri wote ambao wanafanya kazi yako, wanafanya kazi nzuri na ndiyo maana shughuli zinakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na mimi kunipa nafasi name niwe miongoni mwa wachangiaji wa bajeti hii iliyoko mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuishukuru sana kwa dhati Serikali ya Awamu ya Tano kwa mwelekeo wa bajeti hii ambayo imegusa kila sekta, nampongeza sana Rais wetu. Vilevile nimpongeze kwa kumteua Dkt. Mpango na Naibu Waziri, lakini pia na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha. Pia niwapongeze watumishi wote Wizara ya Fedha kwa mwelekeo wa bajeti hii nzuri ambayo imegusa kila mahali, imegusa kila sekta, nampongeza sana Waziri kwa kazi nzuri ambazo mmekuwa mkizifanya hasa bajeti iliyoko mbele yetu. Hongera sana Mheshimiwa Mpango kwa kazi nzuri ambayo iko hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili nizungumzie hizi taulo za kike. Serikali iliondoa VAT kwenye bajeti iliyopita kwa ajili ya kuwasaidia mama zetu, dada zetu na watoto wetu kwa ajili ya taulo hizi za kike. Lakini baadhi ya wafanyabiashara ambao walikuwa sio waaminifu bei haikuweza kupungua. Sasa Serikali imeweka mkakati na mpango mzuri wa kuhakikisha viwanda vyetu vya ndani vinazalisha taulo hizi ili bei ziweze kupungua. Ombi langu kwa Serikali, tusimamie ili lisije likatokea tena kama ambavyo wafanyabiashara kadhaa hawakuweza kupunguza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la wafanyabiashara au wajasiriamali mbalimbali ambao Waziri wakati anawakilisha hapa alisema sasa Serikali haitafunga biashara, haitafunga maduka au biashara mbalimbali za wafanyabiashara hususan wilaya na mikoa kutumia makufuli haya ya TRA. Ombi langu makufuli haya ya TRA, sasa Serikali ihakikishe wilaya na mikoa yatupwe ili kuwapa imani wafanyabiashara, maana Waziri alisema hapa mwenye mamlaka wa kuagiza makufuli haya yafungwe ni Kamishna wa TRA. Sasa ili kuwapa imani wafanyabiashara basi wakufuli haya katika wilaya na mikoa yatupwe kabisa ili kusudi kuwapa imani wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la ukusanyaji kodi liko vizuri, lakini ukienda pale Kariakoo kuna maduka mengi sana. Serikali iangalie Kariakoo sasa imegeuza yale maduka kuna watu wanaweka bidhaa mbele ya milango ya wafanyabiashara, hawa machinga na ndiyo inasababisha sasa baadhi ya wafanyabiashara kufunga maduka nao waweke kama machinga, waweke mbele ya milango. Kwa hiyo, Serikali itakosa kodi kwa wafanyabiashara kwa sababu nao wanafunga sasa. Wanaweka mbele ya maduka. Serikali ifanye utafiti wa kutosha ili kuhakikisha hao wanaoweka mbele ya maduka watafutiwe eneo ili wafanyabiashara waweze kufanya biashara vizuri na kulipa kodi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine Serikali imeweka vizuri utaratibu wa magari haya yanayoagizwa kutoka nje. Ukiingia kwenye system unapata bei ili uweze kuagiza kutokana na kodi ambayo utailipa. Sasa kuna jambo ambalo mimi nashangaa tunaweka kwenye system. Mimi ni miongoni mwao, hivi karibuni mimi nimeagiza magari ambayo yameonesha magari haya kwa mwaka 2012 kodi yake ni hii. Wiki iliyopita magari yamefika, kodi ya gari la mwaka 2012, trekta unit IVECO lilikuwa shilingi 10,300,000 ukiacha kodi zingine, tayari limekwenda shilingi 13,000,000 kwa hiyo ongezeko la shilingi 3,000,000 tofauti na bei iliyoko kwenye system linaathiri sana wafanyabiashara. Ombi langu tuhakikishe bei tuliyoiweka kwenye system na ndiyo hiyo inakuja kulipiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la mwisho ni kuhusu Mkoa wa Njombe, tuna Liganga na Mchuchuma, ni uchumi mkubwa sana katika Mkoa wa Njombe na Tanzania kwa ujumla. Tunashindwa kuelewa ni kwa nini haianzishwi, kama tunakuta mipango Serikali iliyoweka ni mizuri mingi, basi tuhakikishe angalau tuanze kwa kuchimba mkaa kwa sababu kuchimba mkaa kule Mchuchuma na Liganga kunahitaji vifaa viwili tu, caterpillar na dozer, tuanzishe kuchimba ili wananchi wa Mkoa wa Njombe na hususan Wilaya ya Ludewa wajue Serikali ina mpango wa kuhakikisha tunachimba mkaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho niiombe Serikali katika makusanyo sasa ambayo tunaendelea kukusanya katika bajeti hii tunapeleka kwenye halmashauri mapema ili ziweze kufanya kazi iliyokusudiwa ambayo tumepitisha bajeti hapa ndani Bungeni. Kwa mfano kwenye Jimbo langu Serikali imetupa fedha, tumejenga Kituo cha Afya Lyamkena, niombe na kituo kile kimeisha tupatiwe fedha kwa ajili ya vifaa tiba ili Kituo cha Lyamkena kiweze kuwahudumia wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Makambako. Ninaipongeza sana Serikali kwa mipango mizuri ambayo maji, afya na kadhaika, mmekuwa mkisaidia katika nchi hii na hususan Halmashauri yangu ya Mji wa Makambako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana kupitia Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii ya Fedha. Hongera, chapa kazi na kaza mwendo. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niungane na Wabunge wenzangu kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi nzuri anayowafanyia Watanzania kwa miradi mbalimbali ambayo imefanywa katika nchi yetu. Kazi zilizofanywa na Serikali hususani katika nchi yetu ni nyingi na ndiyo maana baadhi ya Wabunge wamesema na mimi naungana nao Mheshimiwa Rais huyu kwa kazi alizozifanya ndani ya miaka minne na zaidi, nadhani kwa sababu tuna ugonjwa huu wa Corona, tuna tatizo pia ambalo limeingia katika nchi yetu hasa miundombinu kuharibiwa na mvua ambazo zimenyesha nyingi sana, imevuruga mipango ya Rais ambayo alikuwa ameipanga katika miaka mitano na katika miaka mitano tena iwe kumi, kwa sababu mipango itakuwa imeharibika kutokana na haya mawili niliyoyataja, nadhani Bunge linalokuja iletwe Katiba hapa aongezewe miaka mitano mingine mbele ili aweze kukamilisha ndoto za Watanzania ambazo amepanga ziweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija na ndugu yangu Mheshimiwa Jafo ambaye ndiye anasimamia Wizara hii, kwa kweli mdogo wangu Mheshimiwa Jafo amefanya kazi kubwa sana, pamoja na wanaokusaidia Naibu Mawaziri wawili, Katibu Mkuu na wataalam wote katika Wizara hii. Ukiangalia ukurasa wa 54 unasema tulikuwa na vituo 535 sasa tuna vituo 968 vikiwepo na vya Makambako. Kwa hiyo, Mheshimiwa Jafo amefanya kazi kubwa sana. Kwa sababu amewafanyia kazi Watanzania naye tunamwombea kwenye Jimbo lake kule asitokee mpinzani upite bila kupingwa pamoja na wanaokusaidia nao wapite bila kupingwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile wapo wasaidizi wa Rais akiwepo Waziri Mkuu, kazi kubwa anayowafanyia Watanzania kwa kuzunguka, jana tu tumemwona alikuwa Zanzibar, anawazungukia Watanzania kutekeleza shughuli ambazo Rais amezipanga. Naye Waziri Mkuu kule Ruangwa, mimi na Wabunge tunakuombea upite bila kupingwa. (Makofi/Vigelelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile na dada yangu Mheshimiwa Jenista kwa kazi anazozifanya namwombea kule Peramiho apite bila kupingwa ili aendelee kuwatumikia Watanzania. Pia Spika wetu Job Ndugai kwa kazi kubwa anayoifanya ndani ya Bunge hili kuwatumikia Watanzania naye tunamuombea apite bila kupingwa. (Makofi/ Vigelegele)

MBUNGE FULANI: Naibu Spika kule Mbeya.

MHE. DEO K. SANGA: Lakini na wewe Naibu Spika mdogo wangu, Mheshimiwa Tulia tunakuombea kule Mbeya upite bila kupingwa ili uweze kuwatumikia Watanzania. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maombi haya, nirudi sasa kwenye Jimbo langu la Makambako.

MBUNGE FULANI: Na wewe upite bila kupingwa.

MHE. DEO K. SANGA: Watanzania wakiwepo wa Jimbo la Makambako nawapenda sana, wanajua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye Jimbo la Makambako. Miradi iliyotekelezwa kwenye jimbo langu ni mingi sana. Ombi langu ni dogo tu kwa Watanzania hususani Jimbo la Makambako.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, tuna mradi mkubwa ule wa fedha za kutoka Serikali ya India kwa mkopo nafuu. Mradi ule tumewaambia wananchi mara nyingi sana na kwa muda mrefu kwamba mradi utatekelezwa. Kwa sababu Wizara inayohusika wako hapa, naomba waone namna ya mradi ule kuweza kuanza katika mji wetu wa Makambako. Tunashukuru kwamba kuna miradi ipo inayoendelea ikiwepo pale Mawande, Lingala, Nyamande na pale Ikeru. Miradi hii inaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, nikija kwenye Vituo vya Afya, ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri, pale kituo chetu kipya cha Lyamkena kimeshafikia asilimia 99. Tunaomba vifaa tiba pamoja na wataalam ili kituo hiki kianze kufanya kazi iliyokusudiwa ikiwepo pia na hospitali ya Halmashauri yetu ambayo imejengwa pale Mlowa na imefikia asilimia karibu 100. Tunaomba kupata vifaa tiba ili ianze iweze kuhudumia Wanamakambako.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile upande wa Kituo cha Afya cha Makambako cha zamani, nimemwambia Mheshimiwa Jafo mara nyingi kwamba hatuna wodi ya wanaume; na wanaume wanaugua. Kwa hiyo, ombi langu tuone namna ya kupata fedha tuwapelekee tuweze kujengewa wodi ya wanaume.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija upande wa umeme wa REA, Waziri mwenye dhamana, haki ya Mungu nitoe neno la shukrani kabisa. Kwenye Halmashauri yangu kimebaki kijiji kimoja tu kupata umeme. Naomba kwa sababu nacho ni kimoja, kiweze kumalizwa. Nacho ni Mtanga. Vijiji vingine vyote tumeshapata umeme. Kwa hiyo, kilichobakia ni maeneo madogo madogo ya Vitongoji kuwapelekea. Kwa hiyo, tunakushukuru sana Mheshimiwa Waziri na timu yako kwa namna ambavyo mnatujali kupitia Rais wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni watu wa NIDA, Waziri mwenye dhamana yuko hapa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, basi baada ya maelezo haya, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Nakushukuru sana, ahsante sana.
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi nami niwe miongoni mwa wachangiaji. Katika kuchangia kwanza nianze kwa kuunga mkono hotuba zote mbili; wakati wa kufunga Bunge na wakati wa Ufunguzi wa Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Bunge linaahirishwa au likihitimishwa, ndiyo kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya CCM chini ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli, jemadari na ndiyo iliyofanya Wabunge wengi turudi hapa ndani, kazi hii! (Makofi)

Katika ufunguzi, mwelekeo huu wa miaka mitano, naomba nichangie na nianze na elimu. Tunapozungumzia elimu bila malipo na ndiyo imefanya watoto wetu wengi wapatikane katika maeneo yetu, ambapo wazazi wao walikuwa hawawezi kuwapeleka shule. Elimu bila malipo kwenye sekondari tunasema, msingi na sekondari, ombi langu kwa bajeti inayokuja na Rais wetu mpendwa, isiwe elimu bila malipo kidato cha kwanza mpaka cha Nne. Inatupa taabu hata sisi Wabunge kule Majimboni wakati fulani kusema. Tunaomba iwe mpaka kidato cha sita yaani kuanzia kiadto cha kwanza mpaka cha sita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunadhani hili linaweza kuwa ni zuri. Tunamwomba Waziri mwenye dhamana katika bajeti ambayo inakuja, hebu tujipange vizuri, tuishauri Serikali kupitia Rais wetu kwamba elimu bila malipo iendelee mpaka mpaka kidato cha Sita, yaani cha Kwanza mpaka cha Sita.Tutakuwa tumekwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wamechangia hapa juu ya mikopo, nilikuwa nafuatilia jana. Kwenye mikopo hii kuna baadhi ya watu ambao watoto wetu hawa wanafadhiliwa na taasisi mbalimbali na baadhi ya watu. Inapofika mahali yule mtu aidha ameshindwa kuendelea kumfadhili na kadhalika; unakuta mtoto amefaulu vizuri Kidato cha Sita na kuendelea anashindwa mkopo na baadaye anakuwa hana mahali pa kwenda kwa sababu wafadhili wake wameshindwa na kadhalika. Nami nina mifano hai mingi, watu mbalimbali na wananchi wanavyokuja kwangu, najua hii iko pia kwa Wabunge wenzangu.Ombi langu, jamani wapewe bila masharti, bila kujua amesoma wapi na kadhalika. Maadamu ana vigezo vya kupata mkopo, apewe bila masharti ya aina yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye suala la umeme, ndugu zangu Waziri mhusika yuko hapa, Mheshimiwa Kalemani. Unajua penye kazi nzuri ambayo mtu amefanya lazima tumpongeze. Amefanya kazi nzuri sana. Ombi langu sasa kwenye jimbo langu, najua na kwa wenzangu, asubuhi tumetoka kuongea, Kijiji cha Mutanga kule, walianza kupeleka nguzo, lakini wamesimama. Ombi kwa Mheshimiwa Waziri, wananchi hawa wapewe umeme wa kule Mtanga na Ingangidung, utakuwa umetusaidia na baadhi ya maeneo, nitawasiliana na Waheshimiwa Madiwani, baadhi ya vitongoji ambavyo leo amezungumzia kwamba ni lazima na vyenyewe sasa tulete ili waweze kupata umeme. Kwa hiyo, nitawasiliana na Madiwani, mwishoni mwa wiki hii nitamkukabidhi maeneo ambayo bado hayajapata umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye afya, kazi iliyofanyika ni nzuri sana ya kujenga vituo, zahanati na kadhalika. Ombi langu, kwenye Jimbo langu la Makambako wananchi wanaonipenda sana, nami nawapenda sana kwa dhati kabisa kabisa; na Rais wao wanampenda sana; ombi langu tumekuwa tukizungumzia habari ya X-Ray na Ultrasound. Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana yuko hapa, hivi kweli Mji wa Makambako ambako ndiyo corridor ya kwenda Songea, Mbeya na wapi, ndiyo Jiji kubwa, hivi hatuna X-Ray. Chumba cha X-Ray tulishakijenga, kipo tayari. Tunaomba katika bajeti tunayokwenda nayo tupate X-Ray, Mheshimiwa Waziri atakuwa ametutendea haki katika Mji wetu wa Makambako.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji; Mheshimiwa Aweso yuko hapa, ambaye ni Waziri wa Maji. Naomba ndugu yangu Waziri; Mawaziri wote wanafanya kazi nzuri, wanaendana na kasi ya mwenyewe, wote! Sasa Mji wa Makambako ndiyo mji mkubwa katika miji yote kwa ukanda. Ndiyo corridor pale jamani; kwenda wapi na wapi kama nilivyosema. Ule mradi mkubwa ambao tunapata mkopo nafuu kutoka Serikali ya India, ni vizuri sasa katika Miji 26 ile na Mji wa Makambako upo, Mheshimiwa Waziri atakapokuwa amesimama hapa atuambie ni lini mradi huo wa maji Makambako utaanza ili nikawaambie wananchi wangu wa Makambako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba leo asubuhi Mheshimiwa Waziri amenijibu kuhusu maji, sasa aseme hapa kwamba maji hayo ni ya mwakani au ni ya mwaka huu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu barabara, naishukuru Serikali kwa Mji wangu wa Makambako, tumepata fedha za lami kilometa 3.5 Mjini pale, tunaishukuru sana Serikali. Hata hivyo, wenzangu wameongelea chombo cha TARURA. Naomba kwenye bajeti hii tutakayoanza, naomba tuongezewe fedha ili barabara zetu ziweze kupitika msimu wote. Kwa hiyo, naomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu hapa kuna maboma mbalimbali ambayo yamejengwa; madarasa, zahanati na kadhalika. Ombi langu, Wizara hasa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo, ahakikishe maboma haya ambayo wananchi wamejenga pamoja na Waheshimiwa Madiwani pamoja na Wabunge tuliomo humu ndani, yanaisha kwa kipindi hiki.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, siyo kwa umuhimu…

NAIBU SPIKA: Muda umekwisha Mheshimiwa. Kengele ya pili imeshagonga.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wameongelea hapa juu ya Rais wetu kumwongezea aidha muda. Kuna watu wengine ni kama dhambi hivi kumwongezea. Ndugu zangu, mtu huyu amefanya kazi kubwa kwa miaka mitano iliyoisha na mipango ya miaka hii mitano, ombi langu hapa ndani, atake asitake tumwongezee muda ili aweze kufanya kazi na kukamilisha mipango yake vizuri katika nchi hii. Kabisa! Ili aweze kufanya kazi yake vizuri ili mipango aliyoipanga iweze kukamilika. Atake asitake, tumlazimishe! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu, nilisema hapa kama mnakumbuka kipindi fulani kwamba China wamefanya hivyo na mahali pengine wamefanya hivyo, siyo dhambi kwa mtu anayefanya vizuri. Hata ninyi Wabunge mliorudi maana yake mlifanya vizuri, ndiyo maana watu walisema tena mrudi, kwa hiyo, siyo dhambi tena kumwongezea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi kwanza nitoe pole kwa Mheshimiwa Rais mama Samia, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Spika na wewe Naibu Spika kwa kuondokewa na kipenzi chetu Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Watanzania kwa ujumla tunajipa pole sana kwa msiba huu mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika sana, kuna baadhi ya watu muda si mrefu, hayati Dkt. Magufuli tangu tumemzika wameanza kuzungumza mambo ya ajabu, nashangaa! Msiba huu uliotukuta mama Samia, Waziri Mkuu wamezunguka nchi hii kututafutia kura sisi, kila mahali Waziri Mkuu amekwenda huku, Makamu wa Rais na ndio ambaye ni Rais amekwenda huko na ndiyo tumerudi hapa Waheshimiwa Wabunge. Leo mtu anasimama na watu wengine kwenye mitandao ya kijamii kumtukana na wengine ni kwa sababu wamekosa vyeo na kadhalika na ndiyo wanaosema maneno ambayo hayaeleweki, vyeo atatoa kwa watu wangapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wamelia, Naibu Spika umelia machozi, Spika wetu amelia machozi, mama Samia mliona analia machozi, Marais wastaafu amelia machozi, Mwinyi amelia machozi, walikuwa wanalilia nini? Wanalia kwa huzuni kwa sababu tumeondokewa na kipenzi cha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo mtu mwingine anasema nilipougua nimepigwa risasi kule Nairobi hakuja kunitazama, alikuja mama Samia. jamani Wabunge tuwe wakweli, hivi ndani ya familia ukimtuma ndugu yako baba au mama si ndio wewe umekwenda kumtazama, sasa alitaka afanyiwe nini, amekwenda Makamu wa Rais ambaye sasa ni Rais kwa kutumwa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Kwa hiyo, lazima tushukuru kwa kila jambo ndugu zangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Wanamakambako au wananchi wa Jimbo la Makambako wamenituma, wanahuzunika sana na wanamtakia kila la kheri mama Samia, pamoja na Waziri Mkuu watekeleze wajibu wa Watanzania.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Deo Sanga kuna taarifa Mheshimiwa Msukuma.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Napenda kumpa taarifa mzungumzaji kuhusiana na machungu yaliyopo kwa Watanzania kwamba, ndiyo maana kuna mzungumzaji amezungumza mchana humu anasema kwamba, baadhi ya Wabunge wakikosoa isionekane nongwa. Sisi tunaona nongwa kwa sababu wakosoaji wote waliokosoa ni watu waliokula viapo, sasa viapo huwa vinaendelea hata kama umetolewa kwenye madaraka. Tutaendelea kuwapiga mpaka watambue umuhimu wa kiapo walichokiapa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Deo Sanga, malizia mchango wako.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nimeipokea taarifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu katika bajeti hii ndio Mtendaji Mkuu wa Serikali, sasa naomba nizungumzie changamoto, kazi kubwa zimefanyika katika Jimbo la Makambako na Tanzania kwa ujumla, lakini kwa leo naomba nichangie changamoto. Changamoto ya kwanza, tuna tatizo la fidia katika Mji wa Makambako, kuna wananchi wanaokaa katika eneo lile la Polisi, wananchi hawa wameanza kuishi pale kabla ya Polisi kupewa eneo lile mpaka sasa wanaishi maisha magumu, hawawezi kuendeleza kufanya kitu chochote.

Naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu na timu yake, Mheshimiwa Jenista dada yangu wahakikishe tunalipa fidia kwa wananchi hawa na IGP Sirro namwamini sana, anafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya pili, katika fidia pale Idofi, Idofi inajengwa one stop center, Serikali imepeleka fedha zaidi ya milioni 800 na kitu, zilizobaki tunaomba zimaliziwe ili wananchi wale waishi kwa amani.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya tatu katika fidia, kuna soko la kimataifa, walilipwa watu zaidi ya bilioni tatu, milioni mia moja na kitu, wamebaki watu kumi na nane, wanapata tabu, tunaomba Serikali imalizie katika kulipa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya nne katika fidia, kuna umeme wa upepo Mheshimiwa Dkt. Kalemani nimekwenda kwake zaidi ya mara mbili. Naomba wakae walitatue tatizo hili la kuwalipa wale wananchi fidia kwa ajili ya umeme wa upepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa afya, tumepewa zahanati nyingi, tumejenga katika Mji wa Makambako, wananchi wamefanya kazi hiyo pamoja na Madiwani, pamoja na mimi Mbunge. Tuna hospitali, tuna kituo cha afya, tunaomba vifaa tiba ili zahanati hizi pamoja na kituo cha afya kipo Lyamkena pale, kiweze kuanza. Tuna hospitali ya Halmashauri na kadhalika, tuna kituo cha afya ambacho kimeanza kujengwa kule Kitandililo ambacho Mheshimiwa Diwani na wananchi wake na mimi Mbunge wao tumeanza kukijenga, tunaiomba Serikali iunge mkono jitihada za wananchi ambazo zimeanzwa kule Kitandililo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho si kwa umuhimu, kwenye Halmashauri yangu ya Makambako, Madiwani posho wanayoipata kwenye kikao ni tofauti na halmashauri nyingine. Naomba Waziri Mheshimiwa Ummy yuko hapa, tafadhali niombe sana kupitia Waziri Mkuu, Madiwani hawa wapewe posho sawa na halmashauri zingine, kwa sababu nikiwatajia hapa wanapata kiduchu na ninajua tatizo lililopo Makambako lipo katika halmashauri nyingi. Niwaombe sana safari hii Madiwani hawa wapewe posho kama wanavyopewa wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Ummy na Manaibu wake, amepata watu wa kazi naye anafanya kazi nzuri. Nawapongeza Katibu Mkuu na timu yake, Bunge linawaamini watafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna miradi ambayo imekuwa ikizungumzwa hapa na Waheshimiwa Wabunge juu ya miundombinu katika miji 45 na Makambako Mji umo. Wamekuwa wakijibu kwamba mikakati na michakato inaendelea. Tunaomba michakato inayoendelea waimalize haraka ili Makambako tuweze kupata soko kubwa na zuri; tupate barabara ambazo zitaletwa na huu mkopo ambapo fedha zitatolewa na Benki ya Dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wamezungumza hapa wenzangu juu ya afya. Mimi naunga mkono kwamba kwenye afya kuna changamoto, hasa upande wa bima. Watu wanashindwa kujiunga na bima za afya kwa sababu wakienda kwenye matibabu hawapati dawa. Kwa hiyo, tunaomba sana ili tupate watu wengi wa kujiunga na bima ya afya tupeleke dawa, hususan katika Jimbo langu la Makambako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna zahanati tatu pale Makambako ambazo zilitengewa shilingi milioni 150, Mheshimiwa Ummy na wasaidizi wake wanajua. Tunaomba fedha hizi ziende ili wananchi wale kwa zahanati ambazo tumeshawaambia shughuli hizi ziweze kukamilika na kuwahudumia wananchi wa Makambako.

Mheshimiwa Spika, katika elimu bajeti hapa inaonesha mtaongeza sekondari za kata katika nchi hii. Niombe na mimi kwenye Jimbo la Makambako kata mbili hazina sekondari. Kata hizo ni Kitisii na Mwembetogwa, tunaomba tupate fedha ili tuweze kujenga sekondari katika kata hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzangu wamezungumzia sana suala la TARURA na mimi nawaunga mkono. Nina barabara pale ya kutoka Makambako – Mulowa – Kifumbe – Mutanga hadi Lupembe. Tunaona kwamba fedha ambazo TARURA wanatengewa ni kidogo sana.

Mheshimiwa Spika, amezungumza jana Mbunge mwenzangu mmoja hapa; ili kuongeza mfuko huu tufanye kama tulivyofanya kwenye Mfuko wa Maji na Mfuko wa TANROADS, tuongeze angalau shilingi 100 kwenye simu kama walivyochangia Waheshimiwa Wabunge jana. Pia tuongeze hata kwenye mafuta shilingi 50, itaongeza mfuko huu kuwa mkubwa ambapo barabara zetu zitatengenezwa vizuri. Mjini Makambako tuna barabara moja ya mjini pale inayopitia Golgota, ilitengenezwa lami kilometa moja, imebaki kilometa moja na kitu, niombe Mheshimiwa Ummy kupitia TARURA barabara hii iishe.

Mheshimiwa Spika, sasa nina suala maalum. Tangu kitokee kifo cha mpendwa wetu, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa kweli mambo ambayo sasa yameanza kuwekwa kwenye mtandao yanahatarisha amani. Ni hatari kwa nchi yetu, ni hatari kwa Taifa letu na vyombo vya usalama vimebaki kimya.

Mheshimiwa Spika, mfano, ukifungua mule unakuta sasa wamemuweka Mheshimiwa Rais wetu Mstaafu Kikwete, Mheshimiwa Katibu Mkuu Mstaafu Kinana, Mheshimiwa Nape na wewe umo, sasa nani atafuata, hii ni hatari! Ni lazima tukemee jambo hili ambalo ni la kutugombanisha Watanzania kwamba watu hawa ni hatari ndiyo waliofanya vitu ambavyo wameandika mule. Hili ni hatari tukiliacha likaendelea, kesho hatujui atawekwa nani.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kikwete apumzike Msoga kule amefanya kazi yake vizuri na Mzee Kinana naye akapumzike. Huyu Mheshimiwa Nape wewe ni shahidi, 2013, 2014 mpaka 2015 wakati wa uchaguzi akiwa na Mzee Kinana walizunguka miaka mitatu kutafuta kura za CCM. Mheshimiwa Nape huyu alikatwa mpaka kiganja na Kinana alipata maumivu ya bega mpaka alikwenda kutibiwa, tuache! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe sasa wameanza kukuweka kwenye mtandao. Jamani Spika wetu anafanya kazi nzuri, tumuache Spika afanye kazi yake. Suala la Bagamoyo Spika alichosema kibaya ni nini? Amesema mikataba ile ijadiliwe, ninyi ndio mna uwezo wa kusema hiki hakifai, hiki kinafaa; Bunge hili. Tunaelewana ndugu zangu, Spika alichosema kibaya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo kwenye mitandao, aah Spika sijui nini…

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, ndugu zangu, niombe tumuache Spika na Naibu Spika waendeshe Bunge hili vizuri.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Mambo ya Ndani. Kwanza nianze kumpongeza sana Waziri wa Mambo ya Ndani na Naibu Waziri na IGP Sirro pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanazozifanya za kutulinda sisi pamoja na mali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mambo kama mawili na la kwanza vitambulisho hivi vya NIDA ni tatizo kubwa sana katika maeneo mbalimbali hususan katika Jimbo langu la Makambako. Watu wameandikisha, wengine wamepata namba lakini vitambulisho vyenyewe hawajapata, kila wanapofuatilia havipatikani. Wengine wanakaa mbali vijijini kwenda wilayani kule nenda rudi nenda rudi, jambo hili limekuwa lina usumbufu mkubwa, nina imani na majimbo mengine katika nchi hii tatizo hili ni kubwa. Kwa hiyo, tunaomba sana katika bajeti hii Waziri aone namna ya kuhakikisha anaondoa usumbufu kwa wananchi juu ya kupata haki zao za vitambulisho vya NIDA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, pamoja na kwamba nimewapongeza kwa kazi nzuri ya ulinzi wanayofanya katika nchi hii, wanafanya kazi nzuri sana lakini hivi sasa vibaka wameanza kunyemelea kurudi taratibu na majambazi wameanza kuteka magari. Nikuombe Waziri na timu yako na IGP Sirro, kama mlivyosimamia jambo hili awali msimamie na sasa ili likome kabisa wananchi waishi kwa amani katika nchi yao na mali zao kwa sababu sasa vibaka wameanza kujitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine liko kwenye Jimbo langu na ni tatizo la muda mrefu. Kituo cha Polisi cha Mji wa Makambako kuna wananchi takriban sita wako ndani ya eneo la polisi; hawaruhusiwi kufanya kitu chochote hata choo kikibomoka hawaruhusiwi kutengeneza. Siku ukipita pale tu hata wewe mwenyewe utawaonea huruma; choo zimebomoka na nyumba zao ziko katika hali mbaya. Niombe fidia ambayo walikuwa wanaidai walipwe ili waweze kuondoka. Nimwombe sana Waziri na IGP Sirro waone namna ya kulipa wananchi hawa sita na tathmini ilishafanywa ili waweze kwenda kutafuta mahala pengine na wao waishi kwa amani katika nchi yao. Chonde chonde sana naomba jambo hili walichukulie kwa umuhimu wake.

Mheshimiwa Spika, Makambako ni center na ni lango kuu la kwenda Songea au Mbeya na sehemu nyingine hata baadhi ya matukio ni watu waliotoka sehemu mbalimbali kuja pale. Kuhusiana na vitendea kazi naomba atenge gari maalum kuja katika kituo cha Makambako ili askari wangu pale waweze kufanya kazi kwa uhakika kulinda wananchi na mali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine tunashukuru kwa kujengewa nyumba za polisi katika eneo letu la Kituo cha Makambako. Haijawahi kutokea kuwa na nyumba pale sasa hivi wametujengea nyumba kwa kweli lazima tushukuru wamefanya vizuri na wananchi ndiyo maana waliunga mkono kujenga nyumba zile za polisi ili walinde mali zao vizuri na mimi Mbunge wao niliunga mkono kuhakikisha nyumba zile zinajengwa.

Mheshimiwa Spika, ombi langu tuendelee kuwajengea nyumba zingine katika bajeti hii ambayo wameitenga ili askari wetu pale waweze kupata nyumba nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo sikuwa na mambo mengi ya kuchangia katika Wizara hii kwa sababu inafanya vizuri ni changamoto ndogo ndogo hizi tulizozizungumzia. La mwisho Mungu aniongoze kwa busara kuna jambo umelisema sasa na mimi kulisema tena siyo vizuri.

WABUNGE FULANI: Sema.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niungane na wenzangu nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niwe mmoja wapo wa kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze sana kwa kumpongeza Jemedari Mkuu Samia kwa kazi nzuri ambayo anaifanya ndani ya nchi yetu. Lakini nimpongeze sana Waziri Kwandikwa kwa kazi nzuri ambayo anaifanya katika Wizara hii ya Ulinzi. Jeshi la Wananchi ni mali ya wananchi na wananchi ni mali yao sasa Kwandikwa namna anavyojichanganya anaendana na jeshi la wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Kwandikwa tunakupongesa sana kwa namna unavyojichanganya na sisi Wabunge wenzako, umekuwa karibu na sisi hongera sana kwa kazi ambayo unaliongoza jeshi hili. (Makofi)

Lakini pili nimpongeze sana CDF Mabeyo, pamoja Makamishna wake wote, kwa kazi nzuri wanayetulinda mipaka yetu na kadhalika, tuko salama tuko kwa sababu wao wapo, wanaliongoza jeshi vizuri kupitia wewe tunakushukuru sana Mabeyo na wenzako kwa kazi nzuri ambayo unaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile niungane na wenzangu kwamba Mabeyo na timu yake na wewe Waziri baada ya kifo cha Jemedari wetu….

NAIBU SPIKA: Jenerali Mabeyo.

MHE. DEO K. SANGA: …kwa kazi nzuri aliyoiongoza kuituliza nchi, juu ya kifo cha kilichotokea cha Dkt. Magufuli amefanya kazi kubwa sana na nitampongeza sana kwa kusimamia mazishi yale chini ya Waziri Mkuu ambaye naye pamoja akisaidiana na Mheshimiwa Jenista, dada yetu kwa kazi nzuri ya kuongoza mazishi yale Jenista tunakupongeza sana kwa kazi nzuri ile ambayo umeifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizo, mimi nina mambo machache, nimesikiliza sana michango ya Wabunge, kuna migogoro baina ya mipaka ya wananchi na jeshi. Ombi langu Mheshimiwa Waziri na timu yako mkae na Waziri Lukuvi na timu yake ili muone muorodheshe maeneo yenye migogoro kati ya wananchi, na jeshi hili yatatuliwe. Litakuwa ni jambo jema sana nitoe mfano mdogo tu pale kwangu Makambako, Mkuu wa Kikosi cha Jeshi la Makambako anafanya kazi nzuri haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yuko jirani na wananchi, anashiriki maendeleo na wananchi, anashiriki kuchangia maendeleo ya shule yetu iko jirani pale ya Kipagamo na maendeleo mengine anafanya, kwa kweli tunampongeza sana Mkuu wa Kikosi chetu cha jeshi pale. (Makofi)

Ombi langu kuna eneo dogo ambalo wananchi walipanda vitindi vya ulanzi. Vitindi ndugu zangu kule kwetu ulanzi ule unagemwa, unaota kutoka chini unagemwa wananchi wanauza, wanapata riziki. Kwa hiyo, sasa wananchi wamekosa kwa sababu jeshi eneo lile wanasema ni mali yao. Ombi langu Mheshimiwa waziri na timu yako tafuta muda, njoo uone eneo linalozungumzwa hili paweze kutatuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nilikuwa na ombi lingine Mheshimiwa Waziri wamezungumzia wenzangu Waheshimiwa Wabunge hapa kwamba Jeshi kwa sababu wanafanya kazi nzuri, wajengewe nyumba nzuri za kuishi. Sasa na mimi nazungumzia juu ya jeshi lililopa Makambako, tuna nyumba ambazo mlizijenga miaka mingi sana za kuishi wanajeshi pale, nyumba hizi hazijamaliziwa zaidi ya miaka 15; nikuombe Waziri fedha ya Serikali iko pale, kuna nyumba zaidi ya tisa, ombi langu nyumba hizi zimalizwe ili wanajeshi waweze kukuaa kwenye nyumba zile. kwa sababu zimekaa hazimaliziwi kwa hiyo niombe sana jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ni kuhusu vijana wanaojiunga kwenda JKT nilikuwa nadhani Serikali itafute namna ambavyo vijana hawa wanapokwenda kujiunga kule, kazi ya JKT ninavyojua mimi ni kwenda kujenga uzalendo wa nchi yao. Sasa tutafute namna ambavyo tuongeze hela/bajeti hili vijana hawa wajiunge kule kwa ajili ya kwenda kujenga uzalendo, tukiacha miaka kadhaa bila ya kupeleka vijana JKT mimi naiona kwamba itakuwa hatari. Waende huko ili wakajenge uzalendo juu ya nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho Mheshimiwa Kwandikwa na timu yako juu ya Jemedari wetu Mama Samia Suluhu Hassan, mimi nawaombea sana kwa Mungu, kwa kazi ambayo mnaifanya ya kulinda nchi hii, mipaka yetu na sisi kwa kweli tuko salama ni kwa sababu yenu. Lakini vilevile pamoja na kwamba si Wizara yake leo pamoja na IGP Sirro na Jeshi lake la Polisi na vyombo vingine vya ulinzi tuko salama ni kwa sababu yao, Mungu akubariki endelea na kazi nzuri ambayo unaifanya ndugu yangu Kwandikwa, ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niwe miongoni mwa wachangiaji katika Wizara hii ya Kilimo. Kwanza, nianze kwa kumpongeza Waziri na Naibu Waziri, Katibu wake na watumishi wote wa Wizara hii. Wizara hii imepata mtu ambaye tunamtegemea sana Waziri pamoja kijana wetu Naibu Waziri, kwa kweli tunawapongeza kwa kazi nzuri ambayo mmekuwa mkiifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi, naunga mkono ushauri wa Kamati ya Kilimo na nadhani muifanyie kazi. Kamati ya Kilimo wameshauri vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie changamoto ambazo zipo nchi nzima au kwenye Mkoa wetu wa Njombe na hususani Jimbo langu la Makambako. Tuna changamoto kwenye zao la mahindi, mahindi katika Mkoa wetu inawezekana na Mikoa mingine ni tatizo kubwa. Mpaka sasa mahindi hayajapata soko, mahindi ya mwaka jana mpaka sasa yapo. Nashauri Wizara ijipange kutafuta masoko ili wananchi wetu waweze kuuza mahindi haya. Wamekuwa wakitupigia simu sana, mahindi yapo kwenye maghala yao mpaka sasa hayajauzwa na hivi sasa kwetu Njombe wameanza kuvuna tena ya msimu huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda Njombe kule mahindi yanauzwa debe Sh.3,000 au Sh.3,500, plastiki ya lita kumi na tisa au ishirini. Kwa hiyo, unakuta sasa uuzaji wa mahindi wa debe hili au gunia hauendani na ununuzi wa pembejeo. Kwa mfano, mbolea ya DAP ndiyo tunatumia sana sisi na mbolea hii ya Urea, mfuko mmoja unauzwa kati ya Sh. 55,000 hadi Sh.60,000, ukijumlisha mifuko miwili unapata Sh.110,000. Katika Sh.110,000 mpaka uuze gunia karibu nne ndiyo ununue mifuko miwili. Kwa hiyo, tunaiomba sana Wizara ione namna ya kukomboa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashauri ili mbolea hii iwe bei chini, Mheshimiwa Waziri tunaimani sana na wewe, Serikali tafuteni wawekezaji ili vijengwe viwanda vya mbolea ya kuzalisha DAP na Urea katika nchi hii hii. Tukipata wawekezaji wa kujenga viwanda vya mbolea, tunaimani mbolea itashuka itaendana angalau na bei ya soko la mazao ambayo wananchi wetu wamekuwa wakiuza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine tuna maghala ambayo mlianza kujenga Dodoma, Makambako na mahala pengine, maghala haya hayajaisha. Ombi letu muhakikishe maghala haya maghala haya yanaisha.

Mheshimiwa Spika, tuna Benki ya Kilimo (TADB), benki hii ipo Dar es Salaam na wakulima wetu kutoka mikoani kule kwenda Dar es Salaam ni mbali. Kwa hiyo, haiwasaidii kabisa vinginevyo inawasaidia watu wenye uwezo mkubwa. Ombi langu ni kwamba benki hii iende katika maeneo husika angalau muitoe Dar es Salaam muweke Dodoma hapa ndiyo katikati. Vilevile mshushe huko kwenye mikoa yetu hasa kwenye mikoa ile ambayo ndiyo inayozalisha mazao ya kimkakati na mazao mengi zaidi ikiwepo Mkoa wa Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile ipo changamoto ya wakulima wetu wa chai, amezungumza sana ndugu yangu hapa Mheshimiwa Swalle ambapo kule Njombe kuna majimbo matatu yanayozalisha chai kwa wingi likiwepo Jimbo la Mheshimiwa Mwanyika, Jimbo la Mheshimiwa Swale la Lupembe na Jimbo la Ludewa. Tatizo kubwa wakulima hawa wameanza kukata tamaa kwa sababu wanacheleweshewa kulipwa fedha zao wanapouza chai, inachukua mpaka miezi minne/mitano hawajalipwa. Kwa hiyo, ombi langu Wizara msimamie kuhakikisha wananchi wanalipwa chai yao wanapouza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Njombe tuna zao kubwa vilevile la parachichi. Parachichi soko lake ni kubwa lakini parachichi hizi zinapozalishwa kule Njombe vifungashio, sitaki nionyeshe vinaonyesha vinatoka nchi gani, vifungashio vile wakifunga inaonekana maparachichi haya hayatoki Tanzania yanatoka nchi jirani. Ombi langu kwa Wizara hebu mfuatilie nchi ambazo zinanunua sana maparachichi na ninyi mjipange kuona moja kwa moja parachichi zinavyotoka Tanzania zinaandikwa parachichi za Tanzania, hii itatusaidia sana katika suala zima la masoko. Sasa hivi watu wanalima kwa wingi sana parachichi, itapendeza kujua soko hili litadumu kwa miaka mingapi na ni nchi gani ambazo zitanunua? (Makofi)

T A A R I F A

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa, ndiyo nimekuona Mheshimiwa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba nchi ya Mexico wanatumia ekari 260,000 kuzalisha zao la parachichi sawa na asilimia 5 ya eneo zima la Mkoa wa Njombe na wanauza parachichi duniani wanapata trilioni 5. Hii maana yake sisi hatujakifanya kilimo hiki cha parachichi kama kilimo biashara. Ahsante.

SPIKA: Unapokea taarifa hiyo Mheshimiwa Deo Sanga kwamba bado msisitizo kwenye parachichi unatakiwa.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, mimi nadhani anasisitiza kwenye suala la kilimo cha parachichi. Kwa hiyo, Waziri amesikia.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante na kengele tayari.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, dakika amenimalizia huyo. (Kicheko)

SPIKA: Hapana, hayajatumia dakika zako, ahsante sana Mheshimiwa Deo Sanga.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niungane na wenzangu. Kwanza nianze sana kwa kumshukuru Rais wetu mpendwa wa Awamu ya Sita Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea bajeti ambayo imegusa na imetii mahitaji ya Watanzania walio wengi, tunampongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili nimpongeze sana ndugu yangu Waziri Mwigulu kwa bajeti hii nzuri pamoja na Naibu Waziri Engineer wetu na Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara hii. Kwa kweli Mwigulu tembea kifua mbele na wasaidizi wako bajeti hii imewagusa sana Watanzania, tunakupongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ambalo nilipenda niliseme; Waheshimiwa Wabunge wengi tupo hapa, tupo mchanganyiko; wapo vijana na kandalika. Ombi langu, mna mipango mingi mbele ya safari. Katika mipango mliyonayo sasa tumuache mama Rais wetu, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wafanye kazi yao, ninyi subirini mpaka 2029 ndipo muendelee na mipango mingine ambayo mnayo huko mbele nadhani mmenielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumuombe Mheshimiwa Waziri na timu yake, kwamba fedha hizi ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezijadili hapa tuombe ziende kwa wakati ili zikafanye shughuli ya maendeleo katika maeneo yetu na katika majimbo yetu. Kwa mfano Wabunge walisema hapa, na mimi nalisema, kwamba yapo madeni ya wazabuni ziende zikalipe. Zipo return za VAT za muda mrefu za wafanyabiashara, mwende mkalipe ili nao walipe madeni ambayo wanadaiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile iko miradi ya maji ambayo Rais wetu na Wizara hii mmedhamiria kumtua mama ndoo kichwani. Sasa kuna miradi ile ya miji 28, na katika miji 28 na Makambaku ipo; mradi ambao fedha inatokana na mkopo nafuu kutoka Serikali ya India; sijajua tumekwamba wapi kwa sababu imechukua muda mrefu. Tuombe, wananchi wana mategemeo makubwa, mkalitatue hili ili kandarasi wawe site waweze kufanyakazi iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ziko fidia ambazo wananchi wamekuwa wakidai. wakiwemo na wa Jimbo langu la Makambaku. Niombe, maana wewe ndiwe bwana kihenge; nikuombe Waziri na timu yako mtoe hizi za fidia ili wananchi waweze kupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la afya na barabara nakadhalika. Kwanza kuna kile wanasema kishika uchumba; nikushukuru Mheshimiwa Waziri kupitia Rais wetu, tumeshapata kwenye majimbo zaidi ya milioni tayari 500 ziko kule, tunakupongeza sana. Kwamba hivi sasa tukirudi au kabla; kwamba TARURA, ukiacha bajeti waliyokuwa nayo tayari milioni 500 wameongezewa. Kwamba pamoja na hili la shilingi mia za mafuta nakadhalika tuna imani zitaongeza maendeleo makubwa upande wa barabara na zitatatua changamoto ambazo zinakumba katika maeneo yetu ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ziko fedha nyingi ambazo tayari hivi sasa zimeenda. Fedha hizi za maendeleo ambazo ziko kwenye force account; fedha hizi Wameshimiwa Madiwani, Waheshimiwa Wabunge kama mlikuwa hamjui, hawaruhusiwi kujua au kushiriki kwa sababu mwongozo unasema anayetakiwa kuwepo kwenye ile force account ni mwananchi mmoja katika kijiji au katika mtaa kwa mradi ule ambao unafanywa katika sehemu ile, na engineer na watu wachache, Diwani haruhusiwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Diwani huyu ndiye badala yetu, ndio Wabunge wa eneo. Sasa Diwani huyu akiulizwa na wananchi hajui, akiulizwa anaambiwa wewe haumo kwenye kamati hii. Niombe sana Mheshimiwa Waziri, ili fedha hizi ziwe salama ni lazima Diwani aingizwe kwenye Mpango huu wa kusimamia shughuli za maendeleo katika eneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nilipenda kwa leo niliseme, TANROADS wanafanyakazi nzuri sana, lakini kuna kipengele kimoja ambacho kimekuwa kandamizi kwa wafanyabiashara, nacho ni hiki; gari likiharibika barabarani au likapata ajali likadondosha oil au mafuta ya diesel au petrol barabarani adhabu yake ni kuanzia milioni 15 mpaka 40 na ushee. Adhabu hii ni kandamizi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa naomba, kwa sababu tunasema tuwawezeshe wafanyabiashara ili waweze kufanya vizuri, ombi langu ni kwamba adhabu hii ikaangaliwe upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna watu wa EWURA wanafanyakazi nzuri kudhibiti mfumuko wa bei za mafuta nakadhalika, lakini nayo iko changamoto ambayo inatakiwa iangaliwe, ni kandamizi kwa wafanyabiashara. Kwa mfano basi linapoingia kujaza mafuta kwenye kituo anatakiwa ashushe abiria, kwamba asijaze mafuta akiwa na abiria. Akipatikana mwenye kituo anamjazia mafuta basi la abiria faini yake ya papo kwa papo ni milioni tatu. Hii ni sheria inayowakandamiza wafanyabiashara, niombe sana iweze kuondoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo Mheshimiwa Mbunge wa Njombe Mjini, ndugu yangu Mwanyika amelizungumza sana hapa; kuhusu Mkoa wetu wa Njombe na kuhusu uwanja wa ndege. Uwanja ule ni uwanja ambao umekuwa kwenye Ilani kwa muda mrefu. tangu mwaka 2005 mpaka leo. Tunaomba; na sisi Njombe, kama alivyosema Mbunge, ni mkoa unaozalisha sana na ni mkoa tunaolima parachichi ambazo zimepata soko la dunia kwenye kilimo hiki cha parachichi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna Liganga na Mchuchuma; na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais jana alivyozungumza nyoyo za sisi wana Njombe na Watanzania yaani tumezuuzika sana. Kwamba Liganga na Mchuchuma imezungumzwa kwa miaka mingi, tatizo ni nini? Tutafute namna ya kulitatua tatizo hili la Liganga na Mchuchuma. Mheshimiwa Joseph Kamonga, Mbunge wa eneo husika amelizungumzia sana. Tatizo ni kulipa fidia za wale watu na kadhalika. Kwa hiyo tunaomba sana, Mheshimiwa Mwigulu tunakuamini sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu suala la hizi benki…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, sekunde. Hizi benki zinatukopesha lakini riba zao ni kubwa Mheshimiwa Mwigulu. Mimi mwenyewe nimekopa juzi, kama mwezi mmoja hivi nimekopa milioni 600. Katika milioni 600 riba ni asilimia 19, hivi tunalipaje? Kipindi kilichopita nilikopa bilioni moja, milioni mia tano thelathini na mbili kwa ajili biashara zangu. Nimemaliza kulipa wamenipa barua ya kunishukuru riba peke yake wameandika kunishukuru pale milioni 918; nitawaonyesheni barua…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana mheshimiwa…

MHE. DEO K. SANGA:…milioni 918 ni bilioni nyingine. Kwa hiyo tunaomba benki waweze kupunguza riba kama ambavyo mama jana amesema ili tuweze kukopa na tuweze kufanyabiashara vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. Kwanza nianze sana kwa kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya kuwaletea Watanzania maendeleo; akiwemo Mtendaji Mkuu, Waziri Mkuu, Makamu wa Rais, ni kazi nzuri sana ambayo inafanywa kuwaletea maendeleo Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwe wakweli Waheshimiwa Wabunge, katika awamu zote ambazo nimekaa hapa Bungeni, hakuna kipindi tulichopata fedha nyingi katika Halmashauri zetu kama hiki. Tumepata fedha nyingi sana maendeleo. Ombi langu, sasa Waziri Mkuu yupo hapa, tumwambie Rais aende akakope tena fedha ili ziweze kujenga vyoo katika mashule yetu, ziweze kujenga nyumba za walimu katika maeneo yetu. Tumekosa nyumba na vyoo katika shule zetu na pia vifaatiba, Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa, katika Vituo vya Afya, Zahanati na Hospitali ambazo zimejengwa. Sasa tukope fedha ili tutimize haya, shughuli ziweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu niwaambie, maendeleo yoyote hayawezi kwenda bila kukopa. Hayawezi kwenda. Hata mimi hapa mjasiriamali, nimekopa mabilioni ya fedha. Lazima ukope ndiyo shughuli zinakwenda. Kwa hiyo, lazima akope ili kusudi ziweze kufanya kazi za maendeleo katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kazi nzuri inayofanywa na Rais, Waheshimiwa Wabunge hawa na Waheshimiwa Madiwani wetu imebidi tuunge mkono jitihada za Rais. Katika maeneo yetu na sisi tumefanya maendeleo katika majimbo yetu. Nikianza na mimi mwenyewe, nimeunga mkono kwa kujenga madarasa tisa hivi sasa ambapo sasa mengine wanapiga ripu, mengine wanaezeka na mengine yamekwisha. Madarasa tisa kwa pamoja. Madarasa hayo ni kama ifuatavyo: Shule ya Kitisi, madarasa mawili; Shule ya Mwembetogwa, madarasa mawili na ofisi; Shule ya Uhuru, madarasa mawili; Shule ya Ilangamoto, darasa moja; Shule la Kifumbe, madarasa mawili. Jumla madarasa tisa. Madarasa hayo yote yatafunguliwa mwezi wa Sita mwaka huu 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, atakayefungua madarasa haya, wa Kwanza namwomba Mheshimiwa Bashungwa, Waziri wa TAMISEMI, aje afungue madarasa mawili na ofisi; Mkuu wa Mkoa, madarasa mawil; Mkuu wa Wilaya, madarasa mawili; Mwenyekiti wa TASAF wa Zanzibar, madarasa mawili ili Muungano uende vizuri. (Makofi/ Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, si hao tu, ASAS wa Iringa kutokana na jitihada za Rais ameunga mkono kwenye Jimbo la Makambako kujenga darasa moja katika Shule ya Magegere. Pia Mbunge mstaafu Haroun Mwambalali ameunga mkono kujenga darasa moja Majengo (Kilimahewa). Kwa hiyo, nawapongeza naomba kupitia kikao hiki Waziri mwenye dhamana wa TAMISEMI peleka barua kwa ASAS na Haroun kuwashukuru kwa kazi nzuri ambayo wameunga mkono jitihada za Rais. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye changamoto kwenye Jimbo la Makambako. Changamoto ya kwanza, kuna tatizo la fidia katika eneo la Polisi, kuna wananchi pale wanapata shida sana, fedha zilikuja wakasema ni kidogo, tukaomba ziongezwe, fedha zile zikahamishwa zikapelekwa Wanging’ombe. Tunaomba wapewe ili kusudi waondokane na tatizo hili. Fidia ya pili, Idofu kunatakiwa kujengwa one stop center wameshalipwa fidia shilingi milioni 800 bado sh.3,100,000,000/=. Ombi langu, tunaiomba Serikali ilete fedha ili waweze kulipwa wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za kujenga mradi mkubwa wa One stop center zipo tayari, Benki ya Dunia ilikwishatoa muda mrefu zili-expire wamerudia tena. Tatizo la tatu ni fidia umeme wa upepo Makambako, wananchi wale walishalipwa bado ambao hawajalipwa, tunaomba kupitia TANESCO waweze kulipa ili wananchi wale waweze kuondoka maeneo ambayo yanahitajika. La mwisho, la nne, soko la Kimataifa, Serikali ilishalipa fidia bado wananchi 18. Kwa hiyo, tunaomba waweze kulipwa ili kusudi kero hii iweze kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tano, wananchi wa Makambako wana matumaini makubwa juu ya miradi ile ya Miji 28. Tunaomba miradi hii imezungumzwa kwa muda mrefu sana. Ombi letu Wabunge tuliopitiwa na miradi hii ya Miji 28, tunaiomba Serikali sasa ifike mwisho miradi hii ianze ili wananchi waweze ku… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, sekunde.

NAIBU SPIKA: Haya sekunde moja.

MHE. DEO. K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho. Posho za Madiwani tunaomba ziongezwe. Madiwani wanafanya kazi nzuri sana za maendeleo katika maeneo yetu, tunaomba posho zao ziongezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Liganga na Mchuchuma tunaomba pia liweze kushughulikiwa. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi nami niwe miongoni mwa wachangiaji. Kwanza naungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwaletea maendeleo wananchi wa Tanzania akisaidiana na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wetu Mheshimiwa Majaliwa Majaliwa Kassim. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nampongeza sana Waziri wa TAMISEMI pamoja na wasaidizi wake wote wawili na Katibu Mkuu na wasaidizi wake wote kwa kazi nzuri wanayoifanya hasa ya kwenda kusimamia miradi ya fedha nyingi ambazo tumezipata kwenye Halmashauri zetu. Hongera sana Waziri na timu yako, tunakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunawaomba wananchi wako wa Jimbo lako watusaidie kuendelea kukuombea, nasi tunakuombea kwa kazi unayoifanya pamoja na wasaidizi wako kuwaletea maendeleo Watanzania. Hongera sana Mheshimiwa Waziri wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nampongeza CEO wa TARURA kwa kazi nzuri anayoifanya kusimamia kitengo hiki cha TARURA. Kwa kweli mimi nasema Waheshimiwa Wabunge wenzangu, anafanya kazi nzuri na tunaomba sasa aongezewe fedha maradufu ili aweze kukamilisha kwenye Halmashauri zetu kufanya kazi nzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, pale upande wa afya, pale Mawande; Kijiji hiki cha Mawande ni kikubwa sana. Kina wakazi wengi sana, lakini hatuna zahanati. Wananchi wale wametoa eneo lao, wamesomba mawe, mchanga uko pale, naomba tupate fedha ili wananchi hawa waweze kujengewa zahanati ili waweze kupata huduma iliyo karibu zaidi, itapendeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile katika Kata ya Utengule eneo la Ikelu nao pia wamekusanya mawe mengi, wamekusanya mchanga, wametengeneza barabara mpaka kwenye eneo lilotengwa kwa ajili kujenga Kituo cha Afya. Naomba tupatiwe fedha ili wananchi hawa weweze kujenga Kituo cha Afya ili huduma iweze kuendelea kutolewa pale.

Mheshimiwa Spika, pia katika Jimbo langu la Makambako, Kata ya Mjimwema, katika bajeti hii tunayokwenda nayo, naomba sana tupewe fedha za kujenga sekondari katika Kata ya Mjimwema. Eneo wanalo, walishatenga, hawana fedha. Nakuomba sana tupewe fedha za kuanzia au za kutimia timu nzima ya kujenga madarasa ya shilingi milioni 600, utakuwa umetusaidia sana katika Kata yetu ya Mji Mwema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzangu wameongelea habari ya Madiwani, niliongea kipindi kilichopita, nirudie tena nami kusema. Madiwani hawa ndio wanaosimamia shughuli za maendeleo katika maeneo yao, wakisaidiana na Wenyeviti wa Vijiji, ndiyo mafiga yanakuwa yamekamilika. Tunaomba sana katika mipango ya Waziri, tunaishukuru Serikali kwa kuwapa Bima ya Afya, ni jambo jema, wamefanya jambo jema zuri sana. Sasa mkae, muone namna ya kuwasaidia kuongeza posho za Madiwani na Wenyeviti wa Vijiji ili timu hii iweze kusimamia vizuri fedha za maendeleo zinazopelekwa huko katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, na hili naomba Waheshimiwa Wabunge mnisikilize vizuri. Sipendi kugombana na taasisi za dini. Kuna mtu mmoja nilimsikiliza juzi juzi hapa akielekezea namna ambavyo amesema kinapofika kipindi cha uchaguzi, CCM tunaiba kura. Nadhani wote mlilisikia hilo. Sasa nasema kwa uchungu mkubwa, mimi nimeshinda kwa kishindo, siyo kwa kuiba kura; na Waheshimiwa Wabunge wote hapa wameshinda kwa kishindo, siyo kwa kuiba kura na Rais alishinda kwa kishindo siyo kwa kuiba kura. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huyu aliyozungumza maneno haya, anataka kutugombanisha na wananchi. Tumeshinda, ndiyo maana hata Jimbo la Sumbawanga tumeshindwa, ameshinda CHADEMA.

MBUNGE FULANI: Nkasi.

MHE. DEO K. SANGA: Nkasi, ameshinda CHADEMA. Kwa hiyo, kuelekezea jamii kwamba CCM wanaiba kura, siyo kweli. Tunashinda kwa kishindo. Watu wanakubali kwa sababu ya haya yanayotekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hivi kwenye maeneo yetu, Rais amepeleka miradi mingi, amepeleka fedha nyingi za maendeleo, watu wanakubali kwa kazi zinazofanyika, ndiyo maana wanatupa kura nyingi. (Makofi)

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Haleluya!

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, ndiyo maana juzi wakati nachangia, nikasema Rais akakope tena fedha ili zifanye kazi ya kujenga nyumba za walimu; za watumishi, vyoo na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, ndiyo nilisema siku ile hapa, ASAS wa Iringa ameunga mkono jitihada za mama, na ndio amesema anajenga darasa moja pale Makambako. Mbunge wa Mbarali naye akaunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais, anajenga darasa moja pale Makambako. Haya ndiyo yanayofanya watu watuchague kwa sababu ya kazi zinazofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye mitandao, watu wameelezea jambo ambalo unashangaa. Wanasema, unaona Mama sasa anaongozwa Mheshimiwa Kikwete. Hivi ni kweli! Kwani Mheshimiwa Kikwete hakufanya kazi nzuri katika nchi hii? Awamu ya Nne Mheshimiwa Kikwete ndio watu walisema fedha zilijaa kwa wananchi, hakufanya Mheshimiwa Kikwete? kwani Mheshimiwa Kikwete ana matatizo gani? Tumwache apumzike vizuri kule Msoga. Tuache habari za kwenye mitandao, tuache Mama afanye kazi ya kuwaletea Watanzania maendeleo. Nimeona niliseme hili kwa hisia kali na kwa sababu watu wanataka kupotosha watu... (Makofi)

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kuhusu utaratibu.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, taarifa. (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Sanga naomba ukae kidogo. Mheshimiwa Halima, Kanuni. (Kicheko)

KUHUSU UTARATIBU

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ambacho nakushukuru Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na timu yako kama nilivyosema, hakikisha wananchi wa Mawande wanapata zahanati; hakikisha Kata ya Utengule eneo la Ikelu wanapata Kituo cha Afya kutokana na kazi ambazo zimefanyika. Diwani wa eneo hili anafanya kazi nzuri sana pamoja na Madiwani wote wa Halmashauri ya Makambako.

Mheshimiwa Spika, naunga mkona hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kuniruhusu na mimi niweze kuchangia. Kwanza nianze sana kwa Kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ndani ya nchi hii. Vilevile nimpongeze pia Waziri Mkuu na msaidizi wake Makamu wa Rais kwa namna ambavyo wamekuwa wakifanya kazi nzuri ya kuunga mkono jitihada za Rais Mama Samia Suluhu Hassan. Vilevile niwapongeze Mawaziri wote kwa namna ambavyo wanavyojituma kuunga mkono jitihada za Rais za kutuletea maendeleo katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, wamesema wenzangu na mimi niungane. Ukweli utabaki kuwa kweli, kuna methali inasema Mnyonge mnyongeni haki yake mpe. Hapa hakuna mnyonge mnyongeni habari ya mnyonge mnyongeni haipo. Mama Dkt. Samia anafanya kazi kubwa, kazi nzuri ya maendeleo katika Halmashauri zetu na nchi hii haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Miradi iliyoko huko kwenye Halmashauri zetu Mabi, na Mabii, na Mabii ni nyingi kwa hiyo tunampongeza sana. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu, fedha zinazokwenda huko ni nyingi na wanaosimamia pia katika Shughuli hizi ni pamoja na Waheshimiwa Madiwani wetu. Naomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu ni lazima tuhakikishe ili wakasimamie vizuri na wenyewe waongezewe posho ili wakasimamie vizuri shughuli za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukulie kwenye jimbo langu la Makambako, ukienda upande wa Maji, miradi iliyofanyika katika jimbo langu ni mingi ya hela nyingi za mabii na Mabii. Vilevile tuna miradi ile ya miji 28 hivi sasa mkandarasi yuko site anaendelea na shughuli za miradi ya maji vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaimani atakapomaliza hivi 2025 Mkandarasi huyu tatizo la maji katika Mji wetu wa Makambako litakuwa limeisha kabisa kwa asilimia zaidi ya100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye Afya, shughuli nyingi nzuri zimefanyika sana katika jimbo letu la Makambako lakini katika nchi nzima. Vilevile ukienda katika upande wa barabara; barabara nyingi zinatengenezwa vizuri hususani pale mjini tuna barabara zinatengenezwa za lami, kuna barabara za Changarawe na Vumbi zinaendelea kutengenezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu TARURA waongenzewe bajeti ili waweze kufanya kazi nzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukinda kwenye elimu, vilevile kwa miaka nenda inapofika Januari, wananchi wetu huwa wanapata tabu kwa namna ambavyo tunakuwa tunawachangisha ili madarasa yaweze kujengwa. Kwenye Halmashauri yetu na nchi nzima tumepata fedha nyingi madarasa yamejengwa na Shughuli zinaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi upande wa elimu, kuna Shule kongwe za msingi ikiwepo Shule ya Mwembe Togwa, Shule ya Mashujaa, shule hizi sasa zinahitaji zipate hela kwa ajili ya ukarabati na kujenga madarasa mengine mapya.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto; pamoja na kazi nzuri mbalimbali ambazo zimefanywa tuna changamoto. Tuna tatizo la fidia eneo la Polisi ambalo Mheshimiwa Rais alipokuja Mwezi Agosti, 2022 wananchi wale wanapata tabu fidia ya Shilingi Milioni 235, wanashindwa sasa waende wapi kwa sababu hawaruhusiwi kuongeza kitu chochote. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali ihakikishe fedha hizi zinatolewa kama alivyoagiza Mheshimiwa Rais ili wananchi hawa waweze kulipwa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye fidia kuna eneo ambalo walipewa fidia zaidi ya shilingi bilioni 3 kwa ajili ya kujenga Soko la Kimataifa, kuna wananchi 18 walibaki hawakulipwa. Tunaiomba Serikali ihakikishe wananchi hawa wanalipwa fidia zao, stahiki zao ili kero hii iweze kuondoka. Hata hivyo, Mheshimiwa Rais alipokuja aliagiza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye fidia kuna tatizo la umeme wa upepo Watu wa muogemo wa upepo walikuja wawekezaji pale na walikuwa tayari kulipa fidia tatizo lipo kwenye wizara ya nishati. Niombe sana Mheshimiwa Naibu Waziri tuhakikishe kwamba hii fidia inalipwa ili wananchi waweze kuishi kwa amani. Nimekuwa nikilizungumza mara nyingi sana jambo hili, na naomba sasa lipate baraka za wananchi hawa kwa kulipwa fidia zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile kuna suala la vifaa tiba. Kwenye halmashauri zetu au kwenye wilaya zetu kwenye hospitali za wilaya tumepata vifaa tiba ambavyo hatujawahi kupata. Tumepata mpaka vifaa ambavyo vinashitua moyo, ambavyo vilikuwa vinapatikana KCMC au Muhimbili. Leo sasa makambako vimekuwepo vifaa hivyo. Kwa hiyo tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. Vifaa ambavyo vilikuwa vinapatikana Ulaya tu leo viko Makambako, vinapatikana; kwa hiyo tunaipongeza sana Serikali kwa kazi nzuri ambayo tumekuwa tukiifanya (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu lingine, kuna barabara ya kutoka Kigoma kwenda Lupembe. Barabara hii tanga 2015 iko kwenye ilani, 2020 iko kwenye ilani. Ombi langu barabara sasa itengewe fedha kwa ajilli ya kutengeneza na wananchi wa lupembe wana imani kubwa kwa sababu rais wetu akiwa Makamu wa Rais aliwaahidi, na sasa tunaomba barabara hii iweze kutengenezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, si kwa umuhimu, ameteuliwa kijana anayeshughulikia mambo ya dawa za kulevya; tunampongeza sana mama kwa kumteua kijana huyo. Ni imani yetu kwamba vijana wetu watapona; akasimamie vizuri suala la madawa ya kulevya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, la mwisho, na Waheshimiwa Wabunge wenzangu hili la mwisho kabisa. Rais Mama Samia yaani hata unapotembea kwenye jimbo lako unatembea unaringa, unajidai kwa sababu mabilioni na mabilioni yamekwenda huko. Na imani yangu, kutokana na mabilioni yaliyokwenda huko Wabunge wote mtarudi na Mama Samia atapata kura nyingi haijapata kutokea kwa sababu ya kazi anazozifanya ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na wewe kwenye jimbo lako yamefanyika kule. Yaani ukipita huku mara upande juu mara ushuke chini na kadhalika na kadhalika, kazi iliyofanyika Dar es salaam ni nzuri, kwa hiyo na wewe tunakuombea, utarudi. vievile Mbeya kwa Spika haijawahi kutokea, ule msongamano wa Mbeya sasa wamepata by-pass ya kupunguza msongamano. Kwa hiyo tunakuombea na wewe Spika na utarudi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo haya nichukue nafasi kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia; lakini kwa kweli mama tunampongeza sana kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niwe miongoni mwa wachangiaji. Maana Wizara hii kubwa ya TAMISEMI ndiyo iliyobeba mabi.. na mabi. na mabi. ndani yake mkiwa na ma... (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu kwamba tunampongeza sana Rais wetu, mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutupatia fedha kupitia Wizara hii. Hela nyingi za maendeleo, zinatisha mabi. na mabi. hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumpongeze sana Waziri, na Naibu Mawaziri wake na wataalam wake wakiongozwa na Katibu Mkuu, kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya. Moja, Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa wewe ni Waziri ambaye umekuwa akipokea simu na wenzake pamoja na Katibu Mkuu; huu ndiyo ukweli. Kwa hiyo, tunampongeza sana sisi wenzake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wenzangu wamempongeza kiongozi wa TARURA; CEO. Kwenye ukweli lazima tuseme ukweli, TARURA wanafanya kazi nzuri sana, ombi letu sisi kama Wabunge, waongezewe fedha ili kwenye majimbo yetu barabara zinapitika, lakini ziweze kupitika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie ajira. Wabunge wenzangu hapa wamezungumzia ajira; mimi naunga mkono kwa sababu majimbo yote yana wasomi, majimbo yote walimu waliomaliza vyuo wapo. Kwa hiyo, tukuombe Waziri na wataalam wako, uone kila jimbo hatutaki kwamba aajiriwe katika eneo analotoka; hapana. Lakini watolewe angalau kila jimbo ili wazazi hawa tunaowasomesha watoto wetu katika sekondari zetu ambazo hizi zimetolewa hela nyingi kujenga wapate imani ya watoto wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya; wakati anawasilisha Waziri hapa nilikuwa namsikiliza kwa makini na Wabunge wenzangu. Rais Dkt. Samia fedha za zahanati peke yake kwa miaka miwili zimeongezeka takribani 1,066; siyo kitu kidogo. Ndani yake na Makambako tumepata zahanati; tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi katika zahanati ambazo wananchi wamejenga, tunaomba zimaliziwe; ni Mkolango, imeisha, Kivavi, Mwembetogwa na Mjimwema. Zahanati hizi wananchi wamejenga kwa kushirikiana na Madiwani na Mbunge wao, tunaomba zipewe fedha ili ziweze kumalizika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vituo vya afya kwa kipindi hiki cha miaka mitatu – nilikuwa nakusikiliza Mheshimiwa Waziri – mama Dkt. Samia ameweza kujenga vituo vya afya 344, ndani yake kuna fedha za tozo vituo 234, kuna fedha za ndani vituo 83, jumla vituo 713; hivi vyote vimebeba maB na maB na maB. Fedha nyingi sana, kwa hiyo, tunakupongeza kwa kusimamia jambo hili ambavyo vituo vya afya viko katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu; kwenye elimu fedha nyingi vilevile wakati unawasilisha hapa zimetolewa za shule za msingi na sekondari. Niombe; kwenye Jimbo la Makambako kuna eneo Kata ya Mjimwema, kata hii ni kubwa, tumeandaa eneo na tumeanza, hatuna sekondari. Kata ya pili ni Kata ya Kitandililo, wananchi wamejenga madarasa matatu, Diwani wao na Mbunge wao nimetia nguvu hapo; tunaomba Serikali iweze kumalizia kuhakikisha Kata hii ya Kitandililo tunatapata sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo haya sasa nizungumzie siasa; amesema Mbunge mmoja kule, Mheshimiwa Kakunda, kwamba mama aliporuhusu mikutano sisi kama viongozi wa CCM tuliguna kidogo. Lakini imeleta tija sana kwa sababu tulifika mahali Waheshimiwa Wabunge tutakubaliana hapa, sisi sote ni Watanzania – tulianza kuogopana. Leo tumekuwa kitu kimoja, ametuunganisha mama, vyama vyetu sasa tunazungumza lugha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tumpongeze sana mama kwa jitihada hizi. Mwezi uliopita nimekwenda Unguja, Pemba, Zanzibar, nimekwenda kule nikakutana na wa vyama vingine, tulikaa tunakula chakula pamoja, tunazungumza maendeleo vizuri pamoja, nikasema Rais Dkt. Samia na Rais Dkt. Mwinyi wanatakiwa kupongezwa sana kwa kutuunganisha Watanzania ambao sasa tunazungumza lugha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi, Mheshimiwa wa Upinzani Mwenyekiti Mbowe, ni lazima naye tumpongeze. Kwa nini nasema tumpongeze; kwa namna maridhiano ambayo wameyafanya. Sasa Mbowe amekuwa naye tunashiriki pamoja, tunaongea pamoja bila tatizo lolote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Mbowe, kwa sababu anataka kuwafanyia maendeleo Watanzania na mama ameshafanya kazi kubwa dunia inamuelewa, 2025 Mbowe tulia muachie mama ili atimize ndoto ya kuwaletea Watanzania maendeleo. Mbowe 2025 shiriki na Madiwani, shiriki na Wabunge, nafasi ya Rais muachie mama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile wapo Wabunge wenzetu pale, wale 19, 20 nadhani na yule wa jimbo. Naomba mnisikilize vizuri, na Mbowe anisikilize vizuri, na Mbowe nilikuwa naye kwenye Kamati ya Katiba 2014, tulikuwa Kamati moja na Mbowe, rafiki yangu. Sasa Mbowe na wenzake kwa huruma ya mama amemsamehe kutoka rohoni, mama Dkt. Samia amesema yote yaliyofanyika nafuta, na yeye wale ni wapiganaji wake walikaa mpaka ndani kipindi fulani, awasamehe. Ni wapiganaji wake, awasamehe. (Makofi/Kigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo gani ambalo mtu huwezi kusamehe kila wakati watoke, watoke; wale ni wapiganaji ambao akina Mheshimiwa Mdee wale walikaa ndani, wakipigana juu ya chama chake, sasa awasamehe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nirudi tena kwenye jimbo. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la soko, Makambako tunasubiri sana, mlishatueleza mtatujengea stendi ya kisasa, mlishatuambia mtatujengea soko la kisasa. Mheshimiwa Waziri hebu tuma timu ya wataalam, tunasubiri kwa hamu ili tuwaoneshe eneo la kujenga soko na eneo la kujenga stendi ili shughuli za maendeleo katika halmashauri yetu ziweze kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kwa kweli ni laizma tumpongeze sana mama kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akifanya, akitupenda Watanzania na dunia imemuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga na Wabunge wenzangu kwamba aijawahi kutokea, nampongeza sana Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuongeza bajeti ambayo haijawahi kutokea mwaka jana bajeti iliongezwa nyingi, mwaka huu yaani ndiyo yameongezwa ma-bi na ma-bi na ma-bi. Kwa hiyo, tunampongeza sana Mama. Vilevile tunampongeza Bashe pamoja na Naibu wake na Katibu Mkuu na watendaji wake wote kwa kazi nzuri wanayoitendea haki Wizara hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu uliyopita tulipopata fedha za ruzuku kule Njombe na najua na wenzangu wengine, Wabunge wenzangu tunakupongeza sana. Mpango huu ndiyo umeongeza mazao ya kilimo mbalimbali kwa sababu baadhi ya wakulima walikuwa wanashindwa kununua mbolea kwa sababu ilikuwa bei juu kutoka shilingi 140,000, shilingi 150,000 leo shilingi 70,000, shilingi 60,000 mfumo ulio uweka tunakupongeza sana. Ombi letu sisi watu wa Njombe mfumo huu uboreshwe, uongezwe mawakala zaidi kwa sababu baadhi ya mawakala walikuwa wachache kwa hiyo hawakufikisha sawa sawa foleni ya wananchi ilikuwa ni kubwa. Kwa hiyo tunakuomba uboreshe mfumo, uongeze zaidi mawakala ili waweze kusambaza mbolea za ruzuku kwa wakati unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekitiki, vilevile lakini kwa Njombe nimpongeze sana Mkuu wa Mkoa Anthony Mtaka kwa namna alivyoungana na wewe kuhakikisha watu wote waliyojaribu kuchanganya mbolea na michanga walikamatwa. Waliyochanganya mbolea feki walikamatwa kwa hiyo tunampongeza sana Anthony Mtaka kwa kushirikiana na wewe kuhakikisha kwamba watu wanaofanya ujanja pamoja na Mkuu wetu wa Wilaya Kisa Gwakisa waliweza kusimamia vizuri zoezi hili la Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile lakini nitaendelea kumpongeza pia Anthony Mtaka sisi Njombe katika Mkoa wetu Wilaya na Makete ndiyo inayozalisha sana ngano. Kwa hiyo tuna washukuru kwa kuunga mkono jitihada za Mkuu wa Mkoa, kwamba sasa Wilaya ya Makete ndiyo kuwe habu ya kulisha Tanzania na nchi ya Tanzania zao la ngano kwa hiyo tunakupongeza sana Waziri kwa kukubali wazo hili na tunampongeza Mama lakini pia Mheshimiwa Waziri Bashe, mtulie vizuri. Wenzangu wamesema hapa wewe ni kijana, wewe ni kijana kweli ubunifu huo unaoendelea nao ndani ya Wizara yako wako watu wengine wanakubeza. Hao wewe songa mbele ndiyo unapatia. Kwa hiyo sisi tunakitakia kila la kheri uweze kufanikisha vizuri katika mpango huu ambao Mama amekutengea fedha nilizosema hapa ma bi na ma bi sasa yanakwenda kuwa na ma ti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho hili siyo liko kwenye Wizara yako Mwigulu Waziri wa Fedha nilimuona hapa. Nikuombe sana Mwigulu mwaka jana mwezi wa nane Rais alipokuja ulikuepo na wewe Bashe ulikuwepo mkumbushane wananchi wa eneo la kituo cha polisi cha Makambako Mjini fidia ambayo unagharimu shilingi milioni 235 na Rais alihaidi pale kwamba fedha hizi zitolewe. Nimuombe Mwigulu sasa muda umefika aweze kutoa fedha hizi ili wananchi hawa waishi kwa amani kwa sababu wanaishi kwa tabu sana nyumba zao zimebomoka, hawawezi kufanya kitu chochote wanategemea uwalipe fidia ili wakaweze kuishi mahala pengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna zao la parachichi Njombe. Mheshimiwa Bashe tukuombe utakapokuwa unamaliza hapa kutoa majibu ya haya Wabunge tuliyochangia unipe na majibu haya sisi Njombe ndiyo wakulima wakubwa wa parachichi Mkoani Njombe. Zao hili kama nyinyi Serikali maana watu wanao nunua wanatoka sehemu mbalimbali muwe na tamko la Serikali kwamba soko lake liko wapi? maana wananchi sasa wamejikita sana kuvunja mashamba yao ya miti na kulima maparachichi sasa isije ikatokea kama Mbunge mwenzangu mmoja amechangia hapa kwamba nchi nzima sasa wamesema walime korosho na sisi hapa isije ikatokea tukalima zaidi parachichi wakati soko kamili hatujapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo akija hapa utuambie soko kamili la parachichi liko wapi? na uhakikishe kinajengwa kiwanda cha parachichi katika Mkoa wetu wa Njombe, cha parachichi ili wananchi wawe na kizazi na kiza kwamba wataendelea kulima parachichi lakini vinginevyo Bashe na timu yako leo nisingependa sana nichangie nakupongeza sana wewe pamoja na Naibu wako pamoja na Katibu Mkuu pamoja na Wizara yote kwa ujumla mshikamane. Sasa kwa mwaka huu wa Kilimo wa 2023/2024 mtakapokuwa mnatuletea mbolea Njombe mtuletee kwa wakati lakini la pili muongeze mawakala kama nilivyosema. Vinginevyo Bashe nakushukuru, endelea na kazi nzuri unaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nami nakushukuru kwa kuniona na kunipa nafasi niweze kuungana na Wabunge wenzangu kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, Wabunge wote hapa waliapata muda wa kuchangia wamezungumzia kwanza, kila aliyeanza anampongeza Rais. Kwa nini tunampongeza Rais? Tunampongeza Rais kwa sababu ana nia njema ya kuhakikisha anamtua mama ndoo kichwani. Ndiyo maana kwenye Wizara hii ameongeza fedha kutoka shilingi bilioni 708 za mwaka jana, mwaka huu ameongeza shilingi bilioni 756. Hizi tunazungumzia siyo milioni, haya ni ma-‘bi’ na ma-‘bi’ na ma-‘b’. Ndiyo maana tunampongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, vilevile tunampongeza aliyekabidhiwa hii Wizara, Amekabidhiwa kijana wetu, Waziri huyu anaitendea haki Wizara. Anaisimamia vizuri pamoja na Naibu Waziri wake. Vilevile wako watendaji wake, yupo Katibu Mkuu wa Wizara na Naibu Katibu Mkuu na Watendaji wote walioko Mikoani na Wilayani akiwemo wa Mkoani kwangu Njombe na Wilayani kwangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Aweso kweli wewe umekabidhiwa dhima hii ya kuhakikisha unamtua mama ndoo kichwani. Ombi langu Waziri, ma ‘B’ haya uliyokabidhiwa yanayokwenda huko kwenye Majimbo yetu yasimamie vizuri yasiliwe. Kazi hiyo unaiweza kwa sababu umedhamiria, tunakuona una nia njema, tunakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika miradi ile ya miji 28 na Mji wa Makambako umo. Katika Mji wa Makambako tumepewa katika miradi wa miji hiyo 28 ma ‘B’ 42. Sasa utakaposimama hapa Wanamakambako wana hamu kukusikia, miradi hii inaanza lini? Useme. Utakaposema waambie Wanamakambako kwamba sasa, maana mradi huu mkubwa wa Makambako unahudumia Kata Tisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, ombi langu utakaposema katika Kata tisa, Kata moja ya Mlowa imo katika hizi Kata Tisa. Katika fedha za kujenga tenki kubwa la kuhudumia, tenki moja linatakiwa liwe kule Mlowa ambalo litahudumia katika kiwanda cha dawa kilichojengwa Makambako, litahudumia katika Hospitali ya Halmashauri yetu iliyojengwa katika Kata hii ya Mlowa na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, tuliomba fedha zaidi ya bilioni tatu na milioni mia tatu kwa ajili ya bajeti ya mwaka huu ili waanze kujenga tenki hilo kubwa la zaidi ya lita 300,000 ili wananchi wa Mlowa kule, Mkolango, Igumila, Idofi pamoja na kiwanda hiki cha dawa waweze kupata maji.

Mheshimiwa Spika, vilevile nikubaliane na ushauri wa Kamati ya Maji na Mazingira. Kamati hii imetoa mapendekezo yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza imeomba mradi wa Bwawa la Mtera uanze ili uweze kuhudumia Dodoma, tatizo la maji Dodoma ni kubwa, kama alivyosema Mheshimiwa Lusinde pale, utakapokuwa unaleta maji Dodoma utahudumia na vijiji vilivyoko njiani. Vilevile Kamati ilishauri pia Dodoma, kwa sababu bado tatizo ni kubwa, vichimbwe visima vya kutosha ili wananchi wa Jiji la Dodoma na kwa sababu linakua kwa haraka waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile Kamati ilishauri uvunaji wa maji. Kamati imeshauri tuhakikishe kuna uvunaji wa maji. Lakini mwenzangu amezungumzia pale sasa elimu hii tuanzie kwenu, tuanzie kwenye majumba ya Serikali. Kamati imeshauri sana juu ya jambo hili. Tunampongeza Mwenyekiti wetu wa Kamati, Mheshimiwa Kiswaga na Wajumbe ambao wametoa ushauri mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, hili halihusiani na Kamati, linahusiana na watu wa Nishati, Naibu Waziri yuko hapa. Kwangu kumekuwa na tatizo kubwa la umeme wa upepo Makambako. Wananchi hawa zaidi ya miaka 14 wamechukuliwa maeneo yao, hawawezi kuendeleza kufanya jambo lolote. Serikali ilisimamisha kwa sababu walipata wawekezaji ambao watawekeza umeme wa upepo Makambako ni jambo jema, lakini mpaka sasa hakuna majibu.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri, leo nimemuunganisha ameongea na wananchi wangu Makambako. Naomba yale uliyowaambia Naibu Waziri yatekelezwe wapate majibu yale uliyowaambia ili kama imeshindikana basi waweze kuruhusiwa kuendelea na mipango yao.

Mheshimiwa Spika, tunapopongeza wote hawa ni lazima tugeuke tukuangalie Spika unayeongoza Bunge hili, tunakupongeza sana kwa kazi nzuri unayoisimamia Bunge, unavyoisimamia Serikali ukishirikana na Wabunge wenzako, tuko pamoja na wewe tutahakikisha shughuli za Bunge hili zinakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, hili namrudia Mheshimiwa Aweso. Unajua Mheshimiwa Aweso - Waziri pamoja na Naibu Waziri na timu nzima ya Wataalam, unapofanya kazi nzuri zipo changamoto, lakini katika chagamoto simamia, songa mbele, nyingine zitakuwa humu, songa mbele unapatia, kazi inakwenda vizuri. Huo ndiyo ukweli kijana. Kimbia hakikisha Majimbo yetu tunamtua Mama ndoo kichwani kama Rais alivyokukabidhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema maneno haya, nakushukuru sana, ahsante sana. Wananchi wa Jimbo la Makambako baadhi ya maeneo maji tunapata tunaendelea vizuri, sitaki nitaje maeneo hayo, maji tulishapata. Ombi langu tu mradi mkubwa huu utakapokuwa unahitimisha uwaambie wananchi wa Makambako mradi huu utaanza lini kwenye Jimbo langu. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Waziri wakati anawasilisha bajeti yake hapa, ameeleza kwamba bajeti kutoka mwaka 2022 mpaka sasa mwaka huu 2023 imeongezeka maradufu. Kwa hiyo, kwa kuongezeka kwa bajeti hii, la kwanza, lazima tumshukuru mama kwa kukuongezea ma-bi na ma-bi na kuwa na ma-ti. Kwa hiyo, tunampongeza sana mama kwa kujali kuongeza bajeti ya Wizara hii ya Mambo ya Ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ameongeza, ni kwa sababu Waziri mwenye dhamana na Naibu Waziri mko vizuri. Ndiyo maana mmeongezewa ma-bi, sasa mmekuwa na ma-ti. Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wako, pamoja na IGP, Afisa Uhamiaji, Makamishna wote pamoja na Katibu Mkuu, kazi mnayoifanya ni kubwa na nzuri sana. Ndiyo maana umesema uhalifu pia kutoka asilimia fulani ya mwaka 2022 na mwaka huu imepungua, ni kwa sababu ya kazi nzuri unayoifanya kuiongoza Wizara hii. Tunakupongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi, unajua Waheshimiwa Wabunge wenzangu, ukitaka kujua kazi ya Jeshi la Polisi na taasisi zake zote wanafanya kazi nzuri, hebu siku moja vituo vya Polisi vifungwe kwa masaa kadhaa, tuone kitakachotokea. Ndiyo maana tunawapongeza, kazi mnayoifanya ni nzuri ya kutulinda sisi na mali zetu. Ongeza jitihada za kuhakikisha unaendelea kutulinda sisi na mali zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri inayofanywa, Mheshimiwa Waziri na timu yako, wapo baadhi ya Askari wanaoliharibia sifa Jeshi la Polisi. Ndiyo maana leo umewaonesha pale zaidi ya watu wanne, umewatunuku kwa sababu ya kufanya kazi nzuri. Kwa hiyo, tunakupongeza kwa kuwatunuku wale kuwa mfano kwa Jeshi la Polisi kufanya kazi nzuri. Wengine pia watakaoendelea kufanya kazi nzuri, wape motisha ili waweze kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ombi. Kituo cha Polisi cha Makambako kina eneo ambalo wananchi walishalitoa. Nimekuelezea mara nyingi, mwaka 2022 mwezi Agosti alipokuja Rais nilisema, wanahitaji fidia yao kwa sababu hawawezi sasa hivi kufanya kazi ya aina yoyote. Hawawezi kuezeka nyumba zao hata kama mabati yameharibika, walizuiliwa. Fidia yao ni Shilingi milioni 250, sito B, ni milioni 235. Nakuomba Mheshimiwa Waziri, jambo hili lichukulie maanani, ukiongea na Waziri wa Fedha ili wananchi hawa waweze kulipwa fidia yao na waweze kuondoka katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la pili, Kituo cha Makambako ni kituo kilichopo center ambapo wako wahalifu wanatoka sehemu nyingine; Songea, Mbeya, Iringa nakadhalika, pale ni kama center. Tunaomba kituo hiki kwa sababu ni kituo kamili cha Wilaya ya Kipolisi, tunaomba vitendea kazi kama magari, kituo cha Polisi chenyewe kiimarishwe, kijengwe vizuri ili waweze kudhibiti uhalifu unatokea katika eneo letu pamoja na Mkoa wetu wa Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, ni lazima tulipongeze Jeshi la Uhamiaji kwa kudhibiti wahalifu wanaoingia nchini. Maana bila kusimamia hawa, ndio wanaogeuka kuwa majambazi na ndiyo wanaotuharibia, lakini Jeshi hili limesimamia vizuri na hatimaye kila wakati tunapata taarifa kwamba wamekamatwa wahalifu mahali fulani, wamekamatwa wahamiaji kutoka sehemu fulani. Kwa hiyo, tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi upande wa Magereza. Makambako tulitenga eneo kwa ajili ya kujenga eneo la Magereza katika Mji wa Makambako. Tunaomba, katika kutenga bajeti yake, Mheshimiwa Waziri aone sasa umuhimu wa kujenga Magereza Makambako ili kupunguza msongamano mkubwa uliopo katika Wilaya ya Njombe. Wilaya ya Njombe ni kubwa sana, kwa hiyo, tunaomba sana utenge fedha kwa ajili ya kujenga Magereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo ambalo wenzangu wamelisema hapa, kwa upande wa NIDA. Vitambulisho hivi vimekuwa tatizo. Baadhi ya watu sasa wanatoka Makambako kwenda kufuata Njombe, na wakifika kule wanaambiwa waje kesho, keshokutwa na nini, kwa hiyo, nadhani tatizo hili inawezekana liko nchi nzima. Tunaomba jambo hili hebu mliwekee umuhimu kuhakikisha raia wa Tanzania wanapata vitambulisho vyao ili wajulikane kama ni raia wetu wa maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumza juu ya malimbikizo ya Askari na mengine, pamoja na kwamba mnakwenda vizuri, hebu mwone namna ya kuhakikisha changamoto hizi za Askari wetu mnaziondoa ili kusiwe na tatizo juu ya Askari wetu ambao wanakuwa wamestaafu na wengine wanakuwa wakati fulani wanadai haki zao. (Makofi)

(Hapa Mhe. Deo K. Sanga alinyamaza kwa sekunde chache)

MBUNGE FULANI: Alikuwa anatafuta ma-bi na ma-bi. (Makofi)

MHE. DEO K. SANGA: Nawashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaona hapa natafuta ma-B, amount ile ili niweze kuitaja hyapa. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiujumla nirudie tena, Waziri kazi yako ni nzuri. Unajua mtu anapofanya kazi vizuri ni lazima tumpongeze. Kabisa, unafanya kazi yako vizuri, pamoja na timu yako ya Makamishna wote pamoja na IGP wako, mnafanya kazi nzuri. Endeleeni. Hawa Askari wachache wanaochafua, mwadhibiti waweze ku…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Sanga.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, vinginevyo naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niungane na Wabunge wenzangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wakati Waziri anawasilisha bajeti hapa nimeisikiliza kwa makini, wakati anawasilisha sikuona kuna mahala ametaja ma-‘bi’, bajeti hii imetajwa ni ma-‘ti’ na ma -‘ti’. Kwa hiyo, tunampongeza sana Mama Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutenga fedha nyingi za miradi katika Wizara hii ya Nishati ya ma -‘ti’ na ma -‘ti’. Tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili tunampongeza Waziri January Makamba pamoja na Naibu wake na Katibu Mkuu pamoja na DG wa REA pamoja na Msaidizi wake na wote wanaotusaidia kazi katika Wizara hii January umeitendea haki Wizara hii unafanya kazi nzuri. Leo Wabunge wenzangu hapa wakati wanachangia wamesema hapa ilikuwa ipitishwe lakini Mheshimiwa Spika akasema kwa utaratibu ni lazima tuseme, tuchangie nakupongeza tena naungana na wenzangu kwa kazi nzuri chapa kazi. Wako watu ambao huwa najiuliza wanapokusoma namna fulani au mnamabifu huko mitaani? Hayo mabifu wayapeleke huko shughuli za Wizara umeiweza kweli kweli chapa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri nije kwenye maombi sasa kwa Jimbo la Makambako, nina maombi machache sana, kwenye Jimbo la Makambako nina maombi mawili, matatu. Ombi la kwanza kuna wale wawekezaji waliokuwa wanakuja kuwekeza umeme wa upepo, jambo hilo limechukua miaka zaidi ya kumi na nane, ishirini. Wananchi wale hawawezi kufanya jambo lolote na kufanya shughuli za maendeleo yeyote yale, nikushukuru walikuja walionana na Wizara yako na watalam wako walikaa, ulimwagiza Naibu Waziri alikutana nao, walizungumza lakini mpaka sasa hatujui kinachoendelea. Nikuombe wananchi wa Makambako Viongozi wanakuja hapa kesho, kesho kutwa watakuwa Bungeni hapa ukutane nao ili uweze kuwapa majibu lakini utakapokuwa unahitimisha kesho pia ni vizuri ukasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kuna Kata ya Mlowa, Makambako pale ni Halmashauri ya Mji, Kata hii kimsingi ni vijiji lakini kwa sababu ni Halmashauri ya Mji hawa wanahesabika wanalipa gharama wananchi wa Mlowa kama mjini gharama za laki tatu na kitu. Ninakuomba tuma timu yako ya watalaam waungane na wasaidizi wako pale Makambako, wakaone hivi ni vijiji typical kabisa wanatakiwa kulipa gharama wanazostahili kulipa wanakijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu katika hilo kuna Kata ya Mahongole, kijiji cha Mpanga, tangu nguzo zimewekwa transformer sasa ni zaidi ya miezi saba haijawahi kuwekwa, ninakuomba wawekewe transformer watu hawa ili waweze kuungana na wenzao kupata umeme. Kwa hiyo, transformer haipo Mtanga, transformer haipo kijiji cha Mahongole, vijiji viwili havina transformer. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine wamezungumza Wabunge wenzangu hapa juu ya gharama hizi za umeme. Mimi nilikuwa nashauri kama mwananchi huyu kulipa gharama ile hawezi, kwanini wasikopesheke wawe wanalipa kidogo kidogo, badala mtu kulipa zile laki tatu kwa wakati mmoja? kwa sababu anahitaji kupata nishati awekewe zile gharama ambazo zinatakiwa kulipwa kila mwezi awe analipa kidogo kidogo mpaka tutapomaliza tutapata wateja wengi kuliko ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine Meneja wangu wa Mkoa wa Njombe wa TANESCO anafanya kazi nzuri sana pamoja na Wasaidizi wake ndani ya Wilaya, Meneja huyu hajathibitishwa na Makambako pale ni TANESCO Kiwilaya lakini anafanya kazi hajathibitishwa kama Meneja wa Wilaya. Kwa hiyo, nikuombe ili wafanye najua hata baadhi ya maeneo inawezekana hicho kitu cha namna hiyo, ninakuomba kama anazo sifa mimi nina imani anasifa, wathibitishwe ili waweze kufanya kazi kwa uhakika za kujituma kwa sababu ni watu ambao tumewaamini na ninyi mmewaamini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine wananchi wa Njombe ambayo sasa umetuwasilishia bajeti hapa, kulikuwa na mradi ule unaitwa Ruhuji wa Njombe, ndugu zangu wa Njombe Serikali ya Mama Samia ikiongozwa chini ya Rais wetu na wasaidizi wake kijana mchapakazi January Makamba na timu yake zimetengwa shilingi huko ndiyo kwenye ma- ‘B’ sasa, zimetengwa shilingi bilioni tano na milioni mia mbili, Tunakushukuru sana mradi huu utawasaidia Watanzania, utasaidia Wananjombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika Njombe kuna Mradi Rumakali uko katika Mkoa wa Njombe Wilaya ya Ludewa huko nako zimetengwa shilingi Bbilionisita na milioni mia mbili na sabini, hiki kitu siyo kidogo! Ndiyo maana tunaposema Mama anaupiga mwingi anastahili sifani kwa sababu ya Ma- B na Ma- B yanayokwenda maendeleo katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwa Mheshimiwa January wamesema wenzangu hapa mradi wa LNG ambao ulikwama kwa miaka saba leo Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan amekukabidhi kazi hiyo. Sasa mradi huu unakwenda kuanza, tunampongeza Mama, tunakupongeza January. Kwamba Watanzania sasa mradi huu ambao ulikwama walikuwa hawana imani sasa tayari wanakwenda, mradi huu unakwenda kuanza na kuwasaidia Watanzania. January Makamba chapa kazi, Mzee Makamba angekuwepo ningesema Mzee Makamba nikupe na zawadi kwa kumzaa kijana huyu, ana maono mazuri huo ndiyo ukweli, penye ukweli lazima tuseme ukweli. Ndiyo maana tunasema Mama amedhamiria Watanzania kuhakikisha anawapa maendeleo katika nchi nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye maji mambo ni Ma- B, ukienda kwenye barabara mambo ni ma-‘bi’, ukienda kwenye elimu mambo ni ma-‘bi’. Leo Bwawa la Mwalimu Nyerere ambalo Kamati hii, Kamati ya Bunge ya Nishati ilikwenda kule Bwawa la Mwalimu Nyerere, leo Wabunge Bwawa la Mwalimu Nyerere tumeliona hapa hapa Dodoma tumeliona Mheshimiwa Makamba tunakutakia kila la kheri na timu yako na Katibu Mkuu wako na Katibu Mkuu yuko imara, huo ndiyo ukweli na DG wa REA na timu yake tunawatakia kila la kheri Mungu ambariki Mama, tuendelee kumuombea achape kazi kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana lakini vilevile na wewe Spika umeliweza kusimamia Bunge tunakupongeza na wewe kwa kazi nzuri unayofanya. Mwenyekiti na timu yako tunawashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naunga mkono hoja kwa asilimia mia mbili.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa bajeti nzuri sana iliyolenga kuwakomboa Watanzania yenye mahela mengi, yenye ma-bi na ma-bi na ma-tri. Kwa hiyo tunampongeza sana Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tumpongeze Mheshimiwa Waziri, Dkt. Mwigulu, kwa bajeti aliyoiwasilisha nzuri, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, Naibu Waziri na timu yako, pamoja na Katibu Mkuu na wataalamu wako; tunakupongeza sana kwa kazi nzuri ambayo unaifanya ndani ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo machache ya kuchangia katika bajeti hii. Kwanza nitoe shukrani kwa fidia ambayo tumekuwa tukizungumzia pale Makambako inayohusiana na polisi; tunakushukuru sana kwa kutupa fidia ile, wananchi wale sasa wameweza kufaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ziko fidia mbili ambazo bado, fidia ya kwanza ni watu wa umeme wa upepe; watu hawa wamesumbuka zaidi ya miaka 20, hatimaye hatujui nani mwekezaji anayewekeza, maeneo yao yamezuiliwa kwa muda mrefu. Tunaiomba Serikali kama haiwezekani basi wananchi hawa waweze kuendelea na maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fidia ya pili inahusu Wizara ya Viwanda na Biashara ambayo walishalipa fidia, kuna baadhi ya watu 18 ambao bado uhakiki wao ulikuwa haujakamilika. Tuombe wakakamilishe uhakiki wao ili waweze kulipwa fidia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni mapendekezo au masuala yaliyokuwa yanawahusu wafanyabiashara. Tunaishukuru Serikali kwa bajeti hii imewajibu mengi mazuri. Lakini nizungumzie mambo mawili; moja ni hili la VAT ambalo lilikuwa linapendekezwa za VAT kutoka shilingi milioni 100 Serikali imejibu sasa itakwenda milioni 200. Ombi langu; fedha milioni 200 kwa sasa ni ndogo, twende mpaka milioni 300 tutakuwa tumekusanya wafanyabiashara wengi ili waweze kujiunga na suala la VAT. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili linahusiana na faini; faini ilikuwa shilingi milioni nne na ushee. Tunaishukuru Serikali imekubali kupunguza maombi ya wafanyabiashara ambayo sasa faini yake wameiweka shilingi milioni tatu. Bado idadi kubwa ya wafanyabiashara hawa, zaidi ya asilimia themanini na kitu, hawana elimu; ombi langu, faini hii ya shilingi milioni tatu bado ni kubwa, siyo suluhisho. Tunaomba angalau sasa iwe milioni moja. Ikiwa milioni moja angalau kwa sababu milioni tatu hela hizi ni nyingi sana kwa faini ya mfanyabiashara ambaye ni mlipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya vitu vinafanyika bila mfanyabiashara kujua kwamba hili amelifanya ni kosa. Kwa sababu kama nilivyosema, wafanyabiashara walio wengi hawana elimu lakini ndiyo idadi kubwa ya wafanyabiashara ambao wako katika nchi yetu. Kwa hiyo, tunaomba bei hii iweze kupunguzwa kutoka amount iliyowekwa sasa iende shilingi milioni moja, ikiwezekana ishuke zaidi, kwa sababu nia ya Serikali siyo kukusanya faini, ni kukusanya kwenye uhalisia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni wakulima wa zao la ngano; bajeti hapa anaelezea Mheshimiwa Waziri alipokuwa anawasilisha HS Code 1001.99.10 na 1001.99.90. Sisi kule Njombe Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa Mtaka, amehimiza wananchi juu ya kulima ngano, Wilaya za Wanging’ombe na Ludewa ni wakulima wa ngano wakubwa ambao wameitikia, na kwa sababu Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Bashe, alihimiza sana kwamba ngano sasa inatakiwa ipatikane kupitia nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukienda Arusha wenzetu wa Arusha nao wameitikia wanalima ngano; ukienda Manyara vilevile wanalima ngano. Sasa kwa kupunguza kodi ngano inayotoka nje kutoka 35 kwenda 10 unawafanya hawa wakulima wa ndani sasa waone hauna umuhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninadhani hii bei 35,000 ya kutoka nje ibaki palepale ili kusudi hawa watu wa viwanda wanunue ngano inayozalishwa hapa, tutakuwa tumewatendea haki wakulima wetu sana. Kwa hiyo, ninaomba sana kwamba Serikali, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, ulione sana jambo hili. (Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Deo Sanga, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Festo Sanga.

TAARIFA

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Hiki anachokizungumza mzee wangu, Mheshimiwa Sanga, ni jambo sahihi kabisa kwa sababu Mheshimiwa Rais, mama Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa Wilaya ya Makete tu ametoa ngano bure kwa wakulima iweze kulimwa kwa ajili ya kusambaza viwandani. Kwa hiyo, kitendo cha kushusha kodi kinakwenda kusababisha kwamba wakulima wetu wawe stranded kwa maana ngano wanayolima sasa itakwenda kukosa soko. Kwa hiyo, hili lazima Wizara ya Fedha iangalie kwa sababu tayari Mheshimiwa Rais ameshachukua hatua ya kushusha na kusambaza ngano bure kwa wakulima nchini, ikiwemo Makete.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Deo Sanga, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili kwa sababu nia ya Serikali ni nzuri, kwamba tuhimize watu wetu ngano izalishwe kwa wingi kupitia Nchini Tanzania, na wakulima wameitikia, na sisi kule Njombe kupitia Mkuu wetu wa Mkoa amehimiza jambo hili, na hata Iringa nao wanalima ngano sana sasa, wameitikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba kwamba Serikali, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, jambo hili liangalie mara mbili, na utakapokuja kwenye majumuisho lazima utupe majibu ili wananchi nchini waweze kujua Serikali imechukuaje hatua juu ya jambo hili ambalo wanategemea kuuza ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho; niishukuru Serikali kupitia Waziri mwenye Dhamana ya Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Dkt. Ashatu, kwa kuweza kulipa fidia ya Liganga na Mchuchuma kule Njombe; tunaishukuru sana Serikali sisi kule Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi letu kwamba sasa fidia imeshalipwa na ni hela nyingi, ombi letu kwamba sasa mradi huu ni lazima Serikali muhakikishe unaanza ambavyo wananchi wa Mkoa wa Njombe na Tanzania kwa ujumla wategemee kwamba Liganga na Mchuchuma sasa inakwenda kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la mwisho; tumepitisha bajeti hapa za kisekta, Wizara mbalimbali; ombi langu kwamba tuhakikishe sasa fedha hizi zinakwenda kwa wakati ili zikaweze kufanya kazi iliyokusudiwa ya maji, barabara, elimu, afya n.k. Kwa hiyo, naomba sana sasa fedha zianze kwenda ili mradi kule wananchi wanategemea sana, na sisi tutakapokwenda kwenye ziara mara baada ya mwisho wa bajeti hii sasa Wabunge nina imani tunakwenda kufanya ziara kwenda kuwaeleza wananchi tulichopitisha hapa fedha za ma-B nama-B na ma-T. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niwe mmoja wa kuchangia katika Wizara hii. Niungane na Wabunge wenzangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuwaletea Watanzania maendeleo; na hata Tuzo aliyoipata hii ni heshima kwetu kubwa sana Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nimpongeze sana Dokta, Waziri wa Ardhi kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na msaidizi wake Ridhiwani Kikwete, mchapakazi, songambele kazi ni nzuri, tunategemea atamsaidia Waziri kufanya kazi nzuri ya kuwaletea maendeleo Watanzania. Vile vile Katibu Mkuu Kijazi na wasaidizi wake, wanafanya kazi nzuri katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nielezee tu machache. Naishukuru Wizara ya Ardhi kwa kutupatia fedha za kupima ardhi, Halmashauri ya Mji wa Makambako, tunawashukuru sana mmefanya kazi nzuri na ndiyo sasa tunaendelea, lakini ombi langu kubwa Mheshimiwa Waziri, wako watu wanaokaimu katika nafasi mbalimbali sasa utendaji kazi unakuwa ni mgumu sana katika Halmashauri nyingi ikiwepo Halmashauri ya Makambako. Afisa Ardhi anakaimu zaidi ya miaka minne, tunaomba sasa athibitishwe ili kusudi afanye kazi yake kwa uhakika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wako watendaji ambao siyo waaminifu. Kwa mfano, kwa maksudi kabisa wako watu ambao wanatoa kiwanja kimoja zaidi ya watu wawili, hii ni hatari sana. Wanagonganisha jamii ya Watanzania watu waanze kuichukia Serikali bila sababu. Tunaomba watu hawa wanaotoa kiwanja kimoja zaidi ya watu wawili wachukuliwe hatua za kinidhamu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo ambayo tuna matatizo ya fidia, hasa nizungumzie Jimbo la Makambako, baadhi ya wananchi imefika mahali aidha warudishiwe maeneo yao. Kwa mfano, eneo la kwanza ambalo lina tatizo ni eneo la Polisi kwa hiyo, tunakuomba Waziri ukae pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani muone namna ya kuwapa fidia hawa wananchi, maana eneo hili limetwaliwa kwa muda mrefu hawajalipwa fedha zao na sasa hawawezi kuendeleza kufanya kitu chochote. Ninaomba sana kwamba, jambo hili liweze kutatuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fidia ya pili ni eneo ambalo lilikuwa lijengwe soko la Kimataifa pale kwetu Makambako. Fidia baadhi ya watu walilipwa, baadhi ya watu 18 hawajalipwa, Wizara ya Viwanda na Biashara ndiyo ilikuwa inashughulikia kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri mkae pamoja ili muweze kutatua tatizo hili la wananchi wa soko la Kimataifa pale Makambako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ni eneo la Idofi ambalo Serikali ilikuwa inajenga One Stop Center imeshalipa fidia zaidi ya Milioni Mia Nane na kitu, bado hela nyingine wananchi kwa muda mrefu hawajalipwa. Ninaomba ukae na Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa Mbarawa ili muweze kutatua tatizo hili wananchi waweze kufaidika na fidia yao ambayo wanaisubiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho katika fidia ni suala la umeme wa upepo, wananchi wa Makambako wanapata shida sana maeneo yale tangu yametwaliwa. Nilikaa na Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Januari Makamba, alisema atalishughulikia. Sasa niombe mshirikiane ili wananchi hawa waweze, kama imeshindikana waweze kurudishiwa eneo lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo Mheshimiwa Waziri napenda niliseme, tunataka Wizara ya Ardhi isimamie mpango bora wa matumizi ya ardhi ili mara nyingine Rais wetu aweze kupewa tuzo ya Kimataifa kutokana na matumizi bora ya ardhi. Tuzo hii atakayoipata itategemea na uchapaji kazi wenu, tuzo hii itakuwa ni faida kwetu Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja, Rais huyu wa Awamu ya Sita ni mteule na Mungu, huo ndiyo ukweli. Sasa siku nyingine nitawaambia kwa kirefu zaidi ili mujue huyu ni mteule na Mungu, leo naomba niishie hapa. Mheshimiwa Waziri chapa kazi, songa mbele, tuna imani kubwa na wewe na timu yako, pamoja na Naibu Waziri wako Mheshimiwa Ridhiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja ya ardhi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi nami niwe miongoni mwa wachangiaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Wabunge wenzangu kwa namna ambavyo tunamshukuru Rais wetu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea bajeti iliyosomwa na Dkt. Mwigulu, bajeti nzuri yenye mwelekeo mzuri kwa ajili ya Watanzania na Majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunasema Mheshimiwa Rais amefanya kazi nzuri? Moja, mpaka hivi sasa, haki ya Mungu kwa muda wa mwaka mmoja haijawahi kutokea fedha nyingi tunazo katika Halmashauri zetu, nyingi sana. Kwa hiyo, tunakushukuru sana. La pili, tukushukuru Dkt. Mwigulu Nchemba pamoja na Naibu wako na Katibu Mkuu wako na Watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri mnayoifanya juu ya kuwaletea Watanzania maendeleo. Mama amefungua milango ya nchi yetu. Kwa hiyo, Dkt. Mwigulu unakwenda katika njia hiyo, hongera, fanya kazi, chapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nawapongeza na Mawaziri wote na Manaibu Waziri kwa kazi nzuri mnayoifanya. Mnaiga mfano, mnafanya kazi nzuri sana. Wako watu hapa ambao wanabeza baadhi ya Mawaziri kwa kazi wanazozifanya. Jamani tuache ubinafsi, tuongee ukweli. Mawaziri mnafanya kazi nzuri, nzuri sana, chapeni kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna suala la maji ambalo katika Miji 28, Serikali zote zilishindwa, haijawahi kutokea, Mama ameweza, tunashukuru sana. Miradi hii ya Miji 28 ikiwepo na Mji wa Makambako, sasa Watanzania na hasa wa Mji wangu wa Makambako, mradi huu ambao tayari umesainiwa, juzi tulikuwa Ikulu, tunashukuru sana. Mheshimiwa Dkt. Mwigulu hakikisha unasimamia fedha ziende kule Makambako zikafanye kazi ya mradi huu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwetu kule Kusini wakulima wetu wana tatizo la mbolea hasa ya DAP na UREA, lakini kutokana na Wizara ya Kilimo, kupitia hili Waziri wa Kilimo alilowasilisha juzi hapa kwamba Serikali sasa itakwenda kutoa ruzuku, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu tunaomba ruzuku hiyo, tunaisubiri kwa hamu ili kusudi mbolea hii iweze kupungua bei. Ni imani yangu kazi hii Mheshimiwa Dkt. Mwigulu utaifanya ili kusudi wananchi wetu waweze kupata mbolea yenye bei nafuu kwa ajili ya wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo sikutaka kuchangia, maana bajeti hii inajieleza, iko vizuri. Iko vizuri! Changamoto kwenye Jimbo la Makambako; tuna fidia ambayo imechukua muda mrefu pale Idofi kwa ajili ya kujenga kituo cha One Stop Center. Serikali imeshatoa fidia zaidi ya Shilingi milioni 870, bado Shilingi bilioni tatu na something. Tunaomba fedha hizo ziende ili kituo cha One Stop Center kiweze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna Kituo cha Polisi Makambako; eneo lile lilozungukwa wananchi pale wanataka kulipwa fidia, zililetwa fedha zaidi ya Shilingi milioni 200, fedha zile baadaye wananchi walipokataa kupokea kwamba ni ndogo na baadaye tulipoongea nao wakakubali fedha zile zikahamishwa zikaenda kujenga Kituo cha Polisi Wanging’ombe. Ombi langu Mheshimiwa Waziri, Hazina toeni fedha sasa walipwe wale wananchi wanateseka sana, sana sana. Kwa sababu ni eneo ambalo muda mrefu limechukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fidia nyingine ya tatu ni suala la Soko la Kimataifa. Serikali ilishatoa Shilingi bilioni 3.1, fedha zilizobaki ni ndogo kwa ajili ya wananchi 18 na wananchi hawa walikuwa wanashughulikiwa na Wizara ya Viwanda na Biashara. Ombi langu sasa, Hazina itoe fedha ili wananchi hawa nao walingane na wenzao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la fidia ni suala la umeme wa upepo. Pia tunaomba Hazina wamalize mazungumzo na TANESCO ili wananchi hawa waweze kulipwa fidia za maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kuna miji 45 ambayo inakwenda kujengwa masoko na stendi ikiwepo na Makambako. Tunaomba Mheshimiwa Dkt. Mwigulu miji hii iweze kuanza hasa ukizingatia pale Makambako ndiyo center ya kwenda Songea, Mbeya, Malawi, na kadhalika. Kwa hiyo, tunaomba jambo hili lianze mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ambalo limezungumziwa kuhusu kulipa magari; malori, mabasi na kadhalika Shilingi 3,500,000/=. Jambo hili Mheshimiwa Dkt. Mwigulu wananchi wamelipokea, wamenipigia sana simu, wanaomba bei ipungue iwe kati ya Shilingi 2,000,000/= na Shilingi 2,500,000/=. Mmelifanya jambo zuri kwamba sasa litakuwa halina longolongo, watu wakishalipa basi, tunakutana mwaka mwingine. Jambo hili wamelipokea vizuri, lakini wanaomba bei ipungue. Shilingi 3,500,000/= ni fedha nyingi. Tunakuomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yako, mkae tena upya, mpange, bei ipungue ili wananchi waweze kumudu kulipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile watu wa vituo vya mafuta nao wanaomba iwe kama hii mliyopanga ya magari. Vituo vya mafuta kwa lita moja wanapata faida ya Shilingi 100/=, na katika faida ya Shilingi 100/= ninyi mnachukua Shilingi 20/= wanabaki na Shilingi 80/=. Halafu mnakuja kukokotoa tena kodi. Kwa nini na wenyewe mnapochukua Shilingi 20/= iwe basi, shughuli imeisha? Litakuwa ni jambo jema sana na mambo yatakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la muda mrefu la hawa waliyosambaza pembejeo, wamekuwa wakidai fedha zao kwa muda mrefu. Ombi langu Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kama watu hawa wapo ambao walikuwa waaminifu, walifanya kazi vizuri, walipwe fedha zao kwa sababu jambo hili limechukua muda mrefu, na Serikali hampo kwa ajili ya kuwadhulumu watu, mpo kwa ajili ya kuwalipa. Tunaomba wale ambao mmehakiki fedha zao, wanatakiwa kulipwa, basi walipwe Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu jambo lingine ni mikopo ya benki. Mikopo hii, naiomba Serikali, benki zetu, ukienda benki nyingine riba ni asilimia 21, wengine 18, wengine 19, wengine 17. Kwa nini isiwe moja? Tunaomba kwenye benki, sisi ni wakopaji, tukope asilimia isizidi 15 ili tuweze kumudu kulipa madeni haya ambayo tumekopa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Deo Sanga. (Makofi)

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niliweke vizuri.

MWENYEKITI: Ahsante, kengele ilishalia.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sekunde moja.

MWENYEKITI: Nilikuongezea, kengele ililia nikaona unaongelea mambo ya muhimu ya benki.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu chapa kazi, fanya kazi na Mama fanya kazi vizuri na Mawaziri wote fanyeni kazi vizuri, mko vizuri na Manaibu Waziri. Ahsanteni sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya Nchi kuhusiana na Umiliki wa Maliasili wa Mwaka 2017.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niungane na wenzangu kuipongeza Serikali ya CCM inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuleta Miswada hii ya Dharura ambayo ndiyo tulikuwa tunaitaka sasa Serikali imetimiza, tunaipongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini unajua mtoto wa kambo hata ungemlisha, ukampa nyama za aina gani atalalamika kwamba hatunzwi. Kwa hiyo, hii sio kitu kigeni, ni kitu cha kawaida tu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Miswada hii kwa kweli ni mizuri sana. Sheria hizi ambazo zitapitishwa Bungeni hapa, sheria zinatoa nafasi kurekebisha hata baada ya kuanza utekelezaji wa mikataba hii. Kwa hiyo, nadhani hili ni jambo jema sana ambalo tumelizungumza sana siku za nyuma. Bunge lililopita tumezungumza juu ya mikataba hii kwamba tunaibiwa, Rais amegundua ametuletea sasa tunataka nini, si ndiyo sasa tuipitishe hapa. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali kwa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile sheria inawapa wananchi kunufaika moja kwa moja na ajira na bima. Pia Halmashauri zetu zitazungumza na mwekezaji kuhusu mahitaji yao, sasa tunataka nini? Kwa kweli jambo hili ni jema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile udhibiti wa maliasili inayopatikana, nia ya Rais wetu kufanya marekebisho kuja haraka inasaidia sana na ndiyo maana leo imeletwa hapa Bungeni. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, pia Miswada hii juzi na jana wadau mbalimbali tumekaa nao pale kwenye ukumbi wa Pius Msekwa. Idadi kubwa ya wadau wameunga mkono sana jitihada za Serikali. Sasa watu wanasema imeletwa kwa dharura lakini imeungwa mkono na wadau mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwakumbushe tu, Miswada ya Habari imezungumzwa zaidi ya miaka 15 na ndiyo juzi juzi tumepitisha hapa, sasa tunataka na hii iwe hivyo? Mimi naunga mkono kabisa Muswada huu ambao umeletwa kwa sababu utaleta manufaa kwa wananchi na kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wengine hapa wanasema Serikali ya CCM 2019/2020 wataingia wengine thubutu, thubutu. Wananchi jambo hili wamelipokea kwa mikono miwili. Kila unapopita, kwanza wanaona tunachelwa. Wananchi wamelipokea jambo hili vizuri na sisi kama Wabunge tuungane ili jambo hili liweze kuanza kwa sababu liko vizuri. Kwanza tunategemea hata zile fedha za makinikia tutapata maji, barabara na kadhalika, kwa hiyo, tumuunge mkono Rais na Wizara kwa ujumla, tusiwakatishe tamaa, sisi tuwe nyuma yao kuhakikisha tunaunga mkono jitihada za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo mengi hapa, unajua wakati fulani huwa nashindwa niseme nini maana Serikali ikileta jambo jema tunasema hapana, sasa tunataka Serikali ifanye nini?

Kuna usemi mmoja unasema shukrani ya nini, sitaki niseme huko, tuiunge mkono Serikali kwa jitihada inazozifanya ili kuhakikisha tunawaletea maendeleo Watanzania. Ili tuhakikishe reli inajengwa, bandari jana tumeona na kadhalika, tunataka tutoke hapo ili tupate uchumi wa kati na mkubwa kwa nchi yetu, kwa hiyo, ni lazima tuiunge mkono Serikali. Kwanza, tunampongeza sana Waziri, Mheshimiwa Profesa Kabudi kwa kuleta Muswada huu na sisi tupo nyuma yako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza imezungumzwa katika sheria hii kwamba itafanya pesa zisipotee kiholela. Vilevile benki za hapa nchini zitatumika kulinda uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono kwa asilimia 400.
Muswada wa Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba ya Maliasili za Nchi wa Mwaka 2017.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niungane na wenzangu kuipongeza Serikali ya CCM inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuleta Miswada hii ya Dharura ambayo ndiyo tulikuwa tunaitaka sasa Serikali imetimiza, tunaipongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini unajua mtoto wa kambo hata ungemlisha, ukampa nyama za aina gani atalalamika kwamba hatunzwi. Kwa hiyo, hii sio kitu kigeni, ni kitu cha kawaida tu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Miswada hii kwa kweli ni mizuri sana. Sheria hizi ambazo zitapitishwa Bungeni hapa, sheria zinatoa nafasi kurekebisha hata baada ya kuanza utekelezaji wa mikataba hii. Kwa hiyo, nadhani hili ni jambo jema sana ambalo tumelizungumza sana siku za nyuma. Bunge lililopita tumezungumza juu ya mikataba hii kwamba tunaibiwa, Rais amegundua ametuletea sasa tunataka nini, si ndiyo sasa tuipitishe hapa. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali kwa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile sheria inawapa wananchi kunufaika moja kwa moja na ajira na bima. Pia Halmashauri zetu zitazungumza na mwekezaji kuhusu mahitaji yao, sasa tunataka nini? Kwa kweli jambo hili ni jema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile udhibiti wa maliasili inayopatikana, nia ya Rais wetu kufanya marekebisho kuja haraka inasaidia sana na ndiyo maana leo imeletwa hapa Bungeni. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, pia Miswada hii juzi na jana wadau mbalimbali tumekaa nao pale kwenye ukumbi wa Pius Msekwa. Idadi kubwa ya wadau wameunga mkono sana jitihada za Serikali. Sasa watu wanasema imeletwa kwa dharura lakini imeungwa mkono na wadau mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwakumbushe tu, Miswada ya Habari imezungumzwa zaidi ya miaka 15 na ndiyo juzi juzi tumepitisha hapa, sasa tunataka na hii iwe hivyo? Mimi naunga mkono kabisa Muswada huu ambao umeletwa kwa sababu utaleta manufaa kwa wananchi na kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wengine hapa wanasema Serikali ya CCM 2019/2020 wataingia wengine thubutu, thubutu. Wananchi jambo hili wamelipokea kwa mikono miwili. Kila unapopita, kwanza wanaona tunachelwa. Wananchi wamelipokea jambo hili vizuri na sisi kama Wabunge tuungane ili jambo hili liweze kuanza kwa sababu liko vizuri. Kwanza tunategemea hata zile fedha za makinikia tutapata maji, barabara na kadhalika, kwa hiyo, tumuunge mkono Rais na Wizara kwa ujumla, tusiwakatishe tamaa, sisi tuwe nyuma yao kuhakikisha tunaunga mkono jitihada za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo mengi hapa, unajua wakati fulani huwa nashindwa niseme nini maana Serikali ikileta jambo jema tunasema hapana, sasa tunataka Serikali ifanye nini?

Kuna usemi mmoja unasema shukrani ya nini, sitaki niseme huko, tuiunge mkono Serikali kwa jitihada inazozifanya ili kuhakikisha tunawaletea maendeleo Watanzania. Ili tuhakikishe reli inajengwa, bandari jana tumeona na kadhalika, tunataka tutoke hapo ili tupate uchumi wa kati na mkubwa kwa nchi yetu, kwa hiyo, ni lazima tuiunge mkono Serikali. Kwanza, tunampongeza sana Waziri, Mheshimiwa Profesa Kabudi kwa kuleta Muswada huu na sisi tupo nyuma yako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza imezungumzwa katika sheria hii kwamba itafanya pesa zisipotee kiholela. Vilevile benki za hapa nchini zitatumika kulinda uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono kwa asilimia 400.