Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Silvestry Fransis Koka (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. SILVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa utendaji usiochelewa. Nasema hivyo kwa sababu tulisimama hapa na tukasema tunahitaji Rais na Serikali ambayo inafanya maamuzi hata kama ndani yake kutakuwa na makosa madogo madogo, naye anafanya hivyo na nina imani tutakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri aikumbuke Kibaha. Tunalo eneo lapata hekta 1,500 lililotengwa kwa ajili ya viwanda na yeye kama alivyo imara kutoa viwanda basi namuomba atoe viwanda hadi eneo hili liweze kukamilika na namuunga mkono kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, malengo ya Tanzania ya Viwanda ni jambo linalowezekana na nia nzuri ya Serikali iliyonayo inawezekana endapo kwa uhakika tutakwenda kuondoa kero na matatizo mbalimbali ambayo yanaturudisha nyuma kwenda kufanikiwa katika azma hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na azma hii tunaiomba Serikali iendelee kutengeneza mazingira bora na rafiki zaidi na wawekezaji na wafanyabiashara. Tunaiomba Serikali iondoe kero mbalimbali ikiwa ni pamoja na tozo za aina moja ambazo sasa zinatozwa na taasisi ambazo ni za usimamizi (Regulatory Authority) utakuta taasisi mbili au tatu zinatoa tozo ambazo zinafanana kwa wafanyabiashara. Hili ni tatizo na ni kikwazo katika uanzishwaji wa viwanda na uendeshaji wa biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna kero nyingine kubwa ambapo viwanda vyetu vya ndani vinapozalisha vinashindwa hasa kushindana na mali zinazotoka nje ya nchi. Hii ni kwa sababu baadhi ya malighafi na utaratibu mzima wa mchakato wa uzalishaji katika viwanda vya ndani vinatozwa kodi, ikiwa ni pamoja na kodi ya VAT. Hii inafanya mali zinazozalishwa na viwanda vya ndani zishindwe kushindana na mali kama hizo zinazotoka nje kwa sababu wao katika uzalishaji hawalipi kodi hizo. Hili ni tatizo kubwa na ningeomba sasa Serikali kupitia Wizara yake ilitazame na kulifanyia kazi ili tuweze kushamirisha nia na madhumuni ya viwanda Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu ni wajibu wa Serikali kulea wafanyabiashara na viwanda, kwa sababu kimsingi Serikali inamiliki asilimia 30 ya makampuni na biashara zote zilizopo ndani ya nchi. Ndiyo maana siku ya mwisho biashara zote zinawajibika kulipa asilimia 30 ya faida inayopatikana na shughuli nzima ya uzalishaji au ya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni wajibu wa Serikali kulea, kutunza na kusaidia ili siku ya mwisho iweze kufaidika na kodi kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. Vivyo hivyo, kwa wafanyabiashara na wazalishaji wanatakiwa wawajibike kwa Serikali na wananchi kwa kutimiza taratibu zote kwa mujibu wa sheria zinazowahusu ikiwa ni ulipaji wa kodi na mengineyo ili kila mmoja aweze kufanya linalofaa na tuwe tunapata win win situation; kwa maana hakika mtu ambaye ana aslimia 30 kama na yeye hutamtimizia haki ni wazi kwamba biashara haitaweza kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu ameonesha nia ya dhati ya kuwasaidia Watanzania, wafanyabiashara na wawekezaji wa Tanzania. Katika mkutano wa Tanzania Business Council uliokaa tarehe 6 mwezi huu, Mheshimiwa Rais alitamka wazi kwamba yupo tayari kuendelea kuwasaidia wawekezaji kwa kuwapa incentives mbalimbali ikiwa ni pamoja na tax holiday ilimradi uwekezaji huo unalenga kunufaisha na kuisaidia nchi, Serikali pamoja na wananchi kwa ujumla wake. Kwa hiyo, ni wazi kwamba nafasi ipo kazi ni kwetu sisi wawekezaji na wafanyabiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu hili ameliweka wazi na amewaagiza watendaji waende wakalitekeleze. Rai yangu kwa wawekezaji, tusilale, rai yangu kwa wafanyabiashara, tusilale. Hatuna sababu ya kuendelea kupata vikwazo kwa sababu Rais amekwisha tamka wazi na yupo tayari kufanya maamuzi yoyote ili lengo na madhumuni ya kuwaunga mkono wafanyabiashara na wawekezaji wa ndani na hata wa nje likamilike.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nichukue nafasi hii kutaka mamlaka zote husika ikiwa ni pamoja na Wizara mbalimbali ziweze sasa kushirikiana na kuhakikisha kwamba azma hii inakwenda kukamilika na tunasonga mbele katika kuimarisha viwanda na vile vile biashara na hatimaye uchumi na maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kifupi sana nizungumzie madeni kwa kuwa kimsingi yanahusika moja kwa moja na biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu mzigo mkubwa wa madeni ya nje na madeni ya ndani ambao Serikali inao, lakini naiomba sana Serikali katika utaratibu wake, ijikite sasa kupunguza mzigo wa madeni ya ndani. Lengo ni lile lile, madeni ya ndani yatakavyolipwa wafanyabiashara na wawekezaji wataendelea kuwekeza na matokeo yake manufaa yale yatakuwa ni kwa ajili ya Serikali na wananchi kwa ujumla wake, ina maana Serikali itaendelea kukusanya kodi kutokana na ile pesa kuingia kwenye mzunguko. Athari ya kupungua kwa ajira itaondoka, maana yake ajira zitaongezeka na hatimaye Serikali itafaidika zaidi pamoja na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Serikali itapata fursa ya kutumia mitaji ya wafanyabiashara na wawekezaji katika kutekeleza malengo na mambo mbalimbali ya maendeleo. Pamoja na hilo uwekezaji wa ndani utaweza vile vile kuvutia zaidi uwekezaji wa nje ambao tunauhitaji ili kwenda kuimarisha uchumi wetu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulipwa kwa madeni ya ndani kutaisaidia Serikali kupata huduma na bidhaa kwa bei nafuu, kwa sababu kunapokuwa na tendency ya Serikali kuchelewa kulipa huduma na bidhaa zinazotokana na wafanyabiashara na za uzalishaji wa viwandani, maana yake ni kwamba kinachofuata huduma zile Serikali itaendelea kuzipata kwa bei ya juu na huku wafanyabiashara wakihofia kwamba ukifanya biashara na Serikali, basi fedha zako zitakaa muda mrefu na ikiwa umezikopa matokeo yake utapata matatizo makubwa. Kwa hiyo, matokeo yake ni kwamba bei zitakuwa ni kubwa na hatimaye hatutafikia malengo ya kubana matumizi na kwenda sambamba katika utoaji wa huduma katika serikali yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kwamba tutasaidia wafanyabiashara wetu, maana wengi tayari wapo kwenye matatizo makubwa na mabenki. Wengine wanafilisiwa na wengine wanapoteza mali zao. Kwa hiyo kwa kuanza kuwalipa wafanyabiashara wa ndani ni wazi kwamba tutachangamsha uchumi na hatimaye wananchi watafurahia na tutasonga mbele kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, madeni ya ndani yakilipwa itawasaidia vile vile Watanzania wengi ambao wanadaiwa kodi waweze kuzilipa kwa wakati na hatimaye siku ya mwisho itakuwa ni win win situation kati ya wafanyabiashara, wawekezaji na Serikali na kimsingi fedha nyingi zitatumika katika kuwekeza na hatimaye tutafikia malengo ya viwanda, ajira na ustawi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na haya machache ya kuishauri Serikali yangu, inaunga mkono hoja asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. SILVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. Nichukue nafasi hii kwanza kuishukuru sana Serikali yetu ya Chama cha MapinduzI kwa kazi nzuri inayofanya. Wizara ya Viwanda imekuwa ikijitahidi kwa hali mali ili kuhakikisha Sera yetu ya Viwanda inakua. Nichukue kweli nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kujitoa na kujitolea kwa ajili ya wananchi wa Tanzania kuhakikisha Watanzania wenyewe tunajenga viwanda na tunakwenda kushika hatamu za uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nitoe pongezi kwa kazi kubwa ya kujenga miundombinu mbalimbali kwa sababu kupitia miundombinu hii ndiyo tunaweza kujenga uchumi wa kati na hata uchumi mkubwa. Mifano iko wazi, ujenzi wa reli, ujenzi wa miundombinu ya umeme kama Stiegler’s Gorge ni jambo ambalo tunahitaji tumuunge Mheshimiwa Rais mkono kwa nguvu zetu zote.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu mojawapo ya changamoto tuliyonayo katika uanzishaji wa viwanda ni pamoja na nguvu za kusukuma au kuendesha viwanda kwa maana ya umeme. Ndugu zangu wote tunafahamu kwamba umeme unaozalishwa kwa maji ni rahisi kuliko umeme mwingine wote. Kwa hiyo, tutakapopata umeme mkubwa unaozalishwa na maji kutoka Stiegler’s Gorge maana yake ni kwamba hata gharama za uzalishaji zitapungua, tutaweza kuzalisha kwa gharama nafuu na hatimaye kufikisha bidhaa kwa wananchi kwa gharama iliyo nafuu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndugu zangu wafanyabiashara wa Tanzania na Watanzania wote tumuunge mkono Rais, tujitokeze tujenge viwanda, tuunge mkono miradi ambayo ipo mbele yetu ili siku ya mwisho jihitada za kwenda kwenye uchumi wa kati ziweze kukamilika bila tatizo lolote.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu ina sababu hasa ya kutazama sasa balance ya biashara ya ndani nje. Tuangalie na tuweze kuona ni namna gani tunapoanza sasa kulea viwanda vyetu tuna balance pamoja importation ya bidhaa muhimu kwa ajili wananchi. Kwa sababu lengo la biashara pamoja na kupata faida na kulipa kodi lakini ni kuwafikishia wananchi bidhaa kwa bei iliyo nzuri, nafuu na ubora. Sasa kama hatutarudi tukaangalia bado kuna watu wachache wata-take advantage na wananchi wataendelea kununua bidhaa kwa gharama kubwa na wao kujilimbikizia faida kubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba kuwepo na balance kati ya bidhaa zinazoletwa kutoka nje na zinazozalishwa ili yale mabadiliko ya bei ya uzalishaji na malighafi yaweze kumnufaisha vilevile mwananchi ambaye ndiye mtuamiaji. Nina imani kwa kufanya hivi tutatimiza azma ya Serikali ya kumhudumia na kumsaidia mwananchi wa kipato cha chini.

Mheshimiwa Spika, kujenga viwanda ni jambo moja lakini kuviendesha ni jambo lingine ambalo ni gumu zaidi. Nitoe mfano wa kiwanda kinachozalisha viuadudu pale Kibaha. Kiwanda hiki kilianza kujengwa mwaka 2010 kikakamilika 2015 na kikaanza uzalishaji 2016. Kiwanda hiki ni cha pekee Afrika na kina uwezo wa kuzalisha viuadudu au viatilifu vinavyoua viluilui vya mbu kiasi cha tani milioni sita kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini navyoongea na wewe kuanzia kilipoanza kufanya kazi mwaka 2016 hadi leo kimezalisha tani laki nne tu na hakuna wanunuzi. Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi kwamba tarehe 22 Juni, 2017

Mheshimiwa Rais alipotembelea viwanda Kibaha alikitembelea kiwanda hiki na alifurahishwa sana na kiwanda hiki kwa sababu ndiyo njia pekee ya kumaliza malaria nchini. Alitoa maagizo kwamba kila halmashauri inunue dawa hii iweze kutumika kuuwa viluilui vya mbu na tuangamize malaria hapa nchini. Tangu kipindi kile katika ya halmashauri 81 ambazo walichukua dawa hii ni halmashauri 25 tu ndizo ambazo zimelipa, nyingine hawajalipa kiwanda kinaendelea kudorora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, dawa hii ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge kama hamuifahamu kazi yake inashambulia viluilui vya mbu katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na maeneo ambayo maji yamesimama na kuhakikisha kwamba mbu hawawezi kuzaliwa. Nafikiri hii ndiyo njia pekee ya kumaliza malaria badala ya kutumia fedha nyingi kununua dawa kwa ajili ya malaria. Dawa hii ni nzuri sana, kwanza kabisa ni environmental friendly, yaani siyo kama dawa nyingine mfano DDT na nyingine tunazotumia kiasi kwamba unaweza hata ukainywa. Watengenezaji wali- demonstrate mbele ya Mheshimiwa Rais kwa kunywa ile dawa, haina hata madhara hata ukiinywa lakini ni sumu kwa viluilui vya mbu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa makusudi kabisa imetenga fedha nyingi kwa ajili ya huduma ya dawa na afya za Watanzania kutoka bajeti ya shilingi bilioni 30 mpaka shilingi bilioni 200 kwa ajili ya dawa ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba malaria inapigwa vita nchini. Sasa tunachoangalia ni watu tumeangukia, ndiyo tunahangaika kutibu malaria hatutaki kuangalia ni wapi tumejikwaa na tutapojikwaa ni kung’atwa na mbu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kama kweli tunataka kusaidia viwanda vyetu vya ndani kiwanda ambacho kimejengwa kwa ushirikiano au kwa msaada kati ya Cuba na Tanzania ambacho hadi sasa tayari wenzetu wa Angola, Nigeria wameshaanza kupata hamu na kuleta order kwa ajili ya dawa hii, tusaidie kiwanda hiki kizalishe dawa na bajeti ya Wizara ya Afya itengwe kwa ajii ya kulipia dawa hizi kwa sababu lengo letu ni kuangamiza mbu si kuendelea kila siku Watanzania wanaugua tunahangaika kuwatibu kwa gharama kubwa. Niombe sana Wizara ya Viwanda na Biashara ishirikiane na Wizara ya Afya ili waweze kununua dawa hizi, Watanzania wapewe elimu ya kuzitumia na hatimaye tuangamize mbu na Tanzania iwe free from malaria. Inawezekana, kiwanda tunacho, tutachekwa kama tutaendelea kuugua malaria na wakati tulishajipanga hadi kuweza kujenga hiki kwa gharama kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiwanda hiki hakijasimamiwa vizuri, kiko chini ya NDC, lakini hadi sasa hakina hata Bodi ya Wakurugenzi sasa kinajiendeshaje? Kina wafanyakazi, uzalishaji ni duni na hakuna anayekiangalia ipasavyo matokeo yake tunakwenda kwenye hasara na tunatoka sasa nje ya azma na sababu ya Tanzania ya viwanda. Ni wazi kama kitasimamiwa kina uwezo mkubwa sana wa kuuza bidhaa hii ndani na hata nje ya nchi yetu na kikailetea Serikali mapato makubwa ya kigeni kwa sababu kiko pekee Afrika na dawa inayotengeneza ni pekee ambayo inakwenda kulenga mbu na kumwangamiza na kuhakiksha kwamba malaria haitaendelea kuwepo.

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja na kuhimiza ujenzi wa viwanda vilevile tushiriki katika kuhakisha viwanda hivi tunavisimamia, tunavisaidia ili viweze kuleta tija na hatimaye tuweze kufikia malengo makubwa ya Tanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuwaasa wafanyabiashara wenzangu Tanzania, kama nilivyosema lengo kubwa la biashara mbali ya kulipa kodi na kupata faida ni kumhudumia Mtanzania. Tuna wajibu wa kuhakikisha tunapopeleka bidhaa katika masoko ya Mtanzania tunamlenga Mtanzania apate nafuu katika bidhaa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameshanyoosha mkono kwa wafanyabiashara, ameamua kutuunga mkono na kutusaidia na hata amekuwa akitoa maamuzi ya papo kwa papo kusaidia wafanyabiashara wa Tanzania. Ametaka wafanyabiashara wa Tanzania tufanye biashara, tuzalishe, tujenge viwanda na tutumie soko la ndani na fedha za ndani kuboresha viwanda vyetu. Sasa kutokupeleka azma hiyo kwa wananchi na kuwafanya wananchi wakawa wanatapatapa wapate wapi mahitaji ni sawasawa na kuiudhi Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimalizie kwa kuomba tujitahidi twende sambamba na azma ya Mheshimiwa Rais na Serikali yetu. Naunga mkono hoja tuendelee kujenga nchi yetu ya viwanda.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SILVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kupongeza na kuishukuru Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa inayoifanya katika miradi mikubwa ya maendeleo, bila kusahau mradi mkubwa wa umeme ambao utatutoa katika matatizo ya umeme wa Stiegler’s Gauge ambao Mheshimiwa Rais ameuvalia njuga na tunamuunga mkono; mradi wa reli ambao utaondoa tatizo la usafiri, ikiwa ni pamoja na Wabunge kuja Dodoma itakuwa ni chini ya saa tatu, tunaunga mkono na tuna imani tutainua uchumi wetu kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa sababu ameendelea kutekeleza miradi mikubwa katika maeneo mbalimbali. Pwani tuna mradi wa barabara, Awamu ya I, kutoka Ubungo mpaka Kibaha ambayo ni six lane pamoja na Daraja la Ubungo. Nilisikia mtu akisema kwamba Daraja la Ubungo halina thamani kwa wakulima vijijini lakini ukweli ni kwamba mazao ya wakulima yanayotoka katika vijiji yatafika Dar es Salaam na yatanunuliwa kwa bei nzuri na mkulima kule atafaidi lakini hata sisi watoto wa huyo mkulima na ndugu zao tutatumia daraja lile na uchumi utachangamka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yote haya yanafanyika kwa ajili ya Watanzania. Mheshimiwa Rais na Serikali yake atajenga miradi hii, haondoki nayo inabaki, tutaendelea kuitumia na atakapomaliza kipindi chake, watoto wetu na wajukuu wetu. Jambo kubwa ni sisi tumuunge mkono Mheshimiwa Rais na Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi na tuishauri iendelee kufanya kazi nzuri ili maendeleo katika nchi yetu yaweze kuja kwa haraka.

Nataka niseme na kumpa moyo Mheshimiwa Rais kwamba hata wafanyabiashara walio wengi sasa voluntarily wanalipa kodi kwa sababu wanaona matokeo ya kodi zao kwamba zinakwenda kufanya mambo makubwa ya maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri tu kwamba katika miradi hii, iko miradi mikubwa na ambayo ni complicated kuiendesha kama Shirika la Ndege na ninajua ndege nyingine zinakuja, tusiogope kushirikisha experts. Tushirikishe experts wenye uzoefu kutoka nje, washirikiane na management ya Kitanzania ili tuweze kufikia malengo na mafanikio ya miradi hii mikubwa. Nina imani kama tuta-blend skills na expertism kutoka nje na ndani ya nchi ni wazi kwamba tutaweza kupeleka mbele gurudumu la maendeleo kwa kuhakikisha miradi hii inakwenda kuleta mafanikio makubwa na kuibadilisha kabisa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka vilevile nizungumzie suala la mazingira ya kufanya biashara. Nafahamu ili mipango hii ya maendeleo iweze kufanikiwa ni lazima mazingira ya ndani ya kufanya biashara yaboreke. Najua Serikali imeshachukua hatua ikiwa ni pamoja na kutengeneza ile blueprint ya kuhakikisha kwamba taasisi zinazohusika na kudhibiti ufanyaji wa biashara zinakuwa ni msaada kwa wafanyabiashara wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachokiomba hapa sasa, Serikali ihimize utaratibu huu, ile blueprint sasa iende kwenye vitendo ili isaidie ukamilishaji na utekelezaji wa miradi hii ya maendeleo na ili kila Mtanzania aweze kufanya biashara katika hali ambayo haina usumbufu na yenye tija. Masuala ya kodi yakae vizuri, masuala ya compliance mbalimbali ikiwa ni pamoja na TBS, TFDA pamoja na taasisi nyingine ziweze kumsaidia mfanyabiashara achangamshe uchumi, kodi zilipwe na hatimaye tufikie malengo yetu. Naomba blueprint sasa iende kufanyiwa kazi na iende kwenye utekelezaji na isiendelee kubakia katika vitabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu imechukua hatua na hatua hii ni hapohapo katika kwenda kuboresha mpango wetu wa maendeleo. Imechukua hatua ya kulinda viwanda vya ndani ikiwa ni pamoja na kuongeza baadhi ya tariffs na imechukua hatua hata ya kupunguza kodi katika bidhaa mbalimbali. Lengo na madhumuni siyo kumfaidisha mfanyabiashara peke yake bali pia kumfaidisha Mtanzania aliye kijijini anayetumia bidhaa zile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini baadhi ya wafanyabishara sasa hawafanyi hivyo, matokeo yake baada ya kuweka tariffs za bidhaa za nje zikaenda juu na wenyewe wanapandisha bei ya bidhaa zao badala ya ku-capitalize katika kuuza zaidi kwa sababu bidhaa zao sasa ni bei rahisi. Niombe sana, azma ya Serikali kufanya hivyo ni kulinda viwanda na kumrahisishia Mtanzania kupata bidhaa kwa bei nzuri na kuhakikisha viwanda vinazidisha uzalishaji. Rai yangu hapa, wenye viwanda na wafanyabiashara walichukue jambo hili au wachukue hili punguzo au ongezeko la bei za bidhaa kutoka nje kuzalisha zaidi na wasiongeze bei kumuumiza yule mlaji wa mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi hii mikubwa ya maendeleo ambayo Serikali imejikita ni wazi kwamba utekelezaji wake unahitaji fedha nyingi na ili fedha ziweze kupatikana ni lazima ulipaji wa kodi uwe mkubwa na ili ulipaji wa kodi uweze kuwa mkubwa ni pamoja na Serikali kwa makusudi kuchangamsha biashara za ndani. Ili biashara za ndani ziweze kuchangamka ni pamoja na kuhakikisha madeni mbalimbali ya wafanyabiashara Serikalini yanalipwa kwa sababu, the main stimulant ya uchumi katika nchi yoyote ile ni Serikali. Katika uchumi wa nchi yetu ulio mdogo ni wazi kwamba mwajiri wa kwanza wa makampuni madogo katika nchi ni Serikali. Kwa hiyo, nina uhakika Serikali ikijikita katika kulipa madeni siku ya mwisho zile fedha zitarudi katika utaratibu wa kodi na uchumi utachangamka na miradi hii itaweza kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii na hakika naunga mkono hoja na tuko pamoja katika kuhakikisha miradi na mipango hii ya maendeleo inatakamilika. Ahsanteni.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. SILYVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi uliyonipangia ya kuchangia. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya katika sekta zote za kuwahudumia wananchi wa Tanzania. Pamoja na kazi nzuri sana inayofanywa na Serikali katika usambazaji wa maji, bado tuna matatizo madogo madogo ambayo hakika wananchi wangu na hususan wa Kibaha Mjini wanakumbana nayo ambapo inawaondolea nafasi ya kufurahia matunda haya ya usambazaji wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Kibaha Mjini, Kata ya Pangani na hususan Mtaa wa Pangani, lakini vilevile Mtaa wa Lumumba, Mtakuja na Miwale wao hawajafaidika na usambazaji wa maji, licha ya bomba kubwa la maji kupita, ambapo linapopita ni chini ya kilometa tatu hadi nne kufikia maeneo hayo. Jambo hili tumelijadili sana na Wizara na kuna mpango wa ujenzi wa tenki la lita 6,000 ambalo litaondoa tatizo katika ule Mtaa wa Pangani na hii mingine kiasi kwamba, hata machinjio yetu ya kisasa yatapata maji. Huu ni mwaka wa tatu kwenda wa nne, kila mwaka mkandarasi anakuja, kila mwaka tenda inatangazwa, jambo hili bado halijafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ni rafiki yangu na ni mchapa kazi, lakini wananchi wa Pangani wanasema bado zile cheche zake za kuchapa kazi hawajaziona. Nimwombe sana, ili tunapofunga bajeti hii tusigombane kwa kushika mshahara wake, basi namwomba atoe majibu sahihi ni lini tenki hili linajengwa, ili wananchi hawa waondokane na adha hiyo kubwa ambayo wamekuwa nayo kwa takribani miaka mitatu minne sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na Kata ya Pangani, lakini tuna maeneo mengine ambayo nayo yana changamoto ya maji ukizingatia Kibaha Mji ni Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani. Kata ya Viziwaziwa kuna uchakavu na kuna msukumo mdogo wa maji. Kwa hiyo, maeneo ya Mitasa, Gare, Viziwaziwa na Mikongeni hawapati maji kwa sababu ya msukumo mdogo, lakini vilevile Kata ya Msangani usambazaji wa maji na hususan, Mitaa ya Kumba, Miembeni na Garagaza nako kuna tatizo kubwa wananchi hawajafikiwa na maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Maili Moja usukumaji wa maji ni mdogo kwa hiyo, wananchi hawapati maji ya kutosha, lakini Visiga, tuna Mitaa ya Saheni, Yerusalemu, Gaza pamoja na Bwawa la Chumvi na kwenyewe bado hawajapata maji licha ya kwamba, hizi ni kata zilizoko katika mji ambao ni Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani. Ombi langu kwa Serikali na kwa Mheshimiwa Waziri, ahakikishe kwamba, pamoja na kazi nzuri ambayo imeshafanyika ya kupeleka mabomba makubwa na kwamba, bomba kubwa linalokwenda Dar-es-Salaam vilevile linapita maeneo haya, sasa basi mgawanyo wa maji haya kwenda katika maeneo haya na msukumo wa maji uzingatiwe, ili wananchi wafurahie matunda ya Mradi mkubwa wa Ruvu Juu na Ruvu Chini kwa ajili ya wananchi wa Pwani na Dar-es- Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni kuhusu mita za maji. Wananchi wengi wanapata adha kubwa kwa sababu ya kupata bili ambazo sio sahihi. Hili limekuwa ni tatizo kubwa kwa muda mrefu katika maeneo mbalimbali. Napenda niishauri Wizara kwamba, kama itachukua hatua zifuatazo nina imani tutaondokana na tatizo hili na hatimaye bili za maji zitakuwa sahihi, hatutakuwa na malalamiko na wananchi watakuwa wanalipa bila kuwa na foleni kubwa ya malalamiko na marekebisho ya bili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tujikite katika teknolojia, kwamba, twende kwenye mita ambazo ni za LUKU. Vilevile ununuzi wa mita na wenyewe una changamoto. Kwa hiyo, ningeishauri Wizara ifanye consolidation kama ni mita ambazo tutakubaliana kwamba, ni kweli zinafaa na ni sahihi, basi zinunuliwe kwa pamoja ili kila mamlaka iweze kupata mita zile na kila mahali katika nchi yetu ambako wanasambaza maji kusiwe na mita ambazo ziko tofauti, hizi zinasoma vizuri, zile zinasoma vibaya, angalau tuwe na mita ambazo zinakubalika na zitakuwa zinatoa usahihi wa ujazo wa maji ambayo yanakwenda kwa wateja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo, kwanza tutaondoa tatizo la upotevu wa maji, lakini pili tutaondoa tatizo la malalamiko na kuwaonea wananchi kwa kuwapelekea bili ambazo hakika hawajatumia maji kiasi kikubwa hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, itafanya hizi mamlaka zetu za maji ziweze kupata fedha bila kutumia gharama kubwa ya kusambaza maji kwamba, kuna watu wanapita kwenda kusoma mita na kutoa makadirio saa nyingine kwa utashi wa mtu kulingana na alivyoona. Kwa hiyo, ningeomba sana hili litiliwe mkazo ili sasa na upande wa maji na yenyewe yasambazwe katika utaratibu wa teknolojia kama tunavyofanya kwenye umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ya kwangu yalikuwa ni hayo machache na naomba nichukue nafasi hii kuunga mkono hoja. Tuko bega kwa bega na Wizara kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata maji. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. SILYVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Wizara yetu muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kipekee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais pamoja na watendaji wake wote kuanzia Wizara hadi Mikoa, hakika ni kazi kubwa inafanyika kwa miradi mikubwa mbalimbali inayofanyika kuanzia viwanja vya ndege, reli, barabara na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada za kutaka kujenga barabara ya express way inayoanzia Kibaha kuja Morogoro na hatimaye Dodoma ambayo itajengwa kwa ubia, hakika hii inakwenda kuwa ni mkombozi wa usafiri kutoka Dar es salaam – Kibaha hadi Dodoma ambayo leo hii unachukua muda mrefu sana na kupoteza muda wa kufanya kazi zenye tija kwa ajili ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, lakini tunazo changamoto mbalimbali katika maeneo yetu na hususani katika Jimbo la Kibaha. Mimi niseme kwamba kazi inayofanywa na TARURA ni kazi inayoleta siasa lakini ni kazi ambayo ina mhudumia mwananchi mpaka eneo lake ikiwa ni pamoja na mitaa katika maeneo mbalimbali na hususani Kibaha Mjini. Pamoja na ujenzi mkubwa wa hizi barabara kubwa, lakini bado wananchi wetu wanapata adha kubwa sana kwa kukosa barabara zinazoingia katika mitaa yao na wakati mvua zikinyesha wanakuwa na changamoto kubwa sana ya kufanya shughuli za kiuchumi na ukizingatia Kibaha ni Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo barabara inayotoka Sheli - Maili Moja - Shule hadi Muheza; barabara hii mvua zikinyesha haipitiki ingawa iko katikati ya Mji wa Kibaha ambao ni Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani; lakini tunayo barabara ya Tumbi – Boko Timiza, tunayo barabara ya Kwa Mathias hadi Mikongeni ambako kuna Makao Makuu ya Chuo Kikuu Huria, lakini vilevile tunayo barabara ya Kongowe – Forestry mpaka Yombo ambayo inaunganisha Kibaha na Bagamoyo, lakini Kongowe - Soga na Visiga - Madafu hadi Mbwawa; hizi ni barabara ambazo ziko ndani ya Mji wa Kibaha na ni barabara muhimu ambazo ningeomba ziko katika network ya TARURA. Sasa TARURA wapewe fedha waweze kuhudumia barabara hizi ili ziweze kutengeneza uchumi katika miji wetu wa Kibaha na ili ziweze kuleta tija kwa wananchi ambao wanataabika sana hasa mvua zinaponyesha, wanashindwa kufanya kazi zao za kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa TANROADS kazi zinaendelea kuwa nzuri, lakini bado kuna maeneo mbalimbali ambayo tunaendelea kusuasua. Barabara ya TAMCO - Mapinga kweli ujenzi unaendelea lakini unakwenda kwa kasi ndogo sana, lakini tunayo barabara ya Makofia – Mlandizi kupitia Mbwawa hiyo barabara iko katika Ilani toka mwaka 2015 na kila mwaka inasemekana fedha zinatengwa, lakini utekelezaji haufanyiki. Mwaka huu tunaona kwamba zimetengwa fedha kidogo sana takribani shilingi milioni 600; sasa fedha hii itafanya nini? Italipa fidia, itaanza ujenzi au itafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niombe kwamba sasa tunapokwenda katika miradi mikubwa na ya kimsingi kama hii ya kuunganisha mikoa basi fedha itoke ya kutosha ili ifanye jambo ambalo litaleta tija na kuonekana machoni mwa watumiaji ikiwa ni pamoja na wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunayo Kisarawe road, barabara ambayo inatakiwa itoke pale Kibaha Mkoani ambayo itatuunganisha na Kisarawe na yenyewe hii imekuwa katika upembuzi yakinifu, bado haijaweza kuanza ujenzi. Naomba barabara hii ijengwe ili iweze kuunganisha Wilaya ya Kisarawe pamoja na Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani ambayo ni Kibaha Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo tunayo barabara ya zamani kwa jina maarufu barabara ya Zamani. Barabara hii inaanzia pale Picha ya Ndege hadi Mlandizi; hii ni barabara ambayo naweza nikasema ni barabara muhimu na ambayo inasaidia sana hasa tunapokuwa na matatizo katika hiyo barabara kuu ya Morogoro. Ninyi ni mashahidi kunapokuwa na ajali katika barabara hii magari hayawezi kupita na ucheleweshwaji unakuwa ni mkubwa sana, hata kama kuna majeruhi kuwakimbiza hospitalini Tumbi inakuwa ni changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hiyo barabara ni mkombozi katika katika jambo hilo kwamba ni barabara iliyokuwepo toka zamani na inahitaji tu ukarabati wa kawaida, sasa ukarabati umeanza kidogo, kidogo na kwa mafungu. Mimi nilikuwa naomba kwamba basi TANROADS ikarabati barabara hii ambayo itakuwa ni mbadala na kupunguza vilevile msongamano katika hiyo barabara kubwa ya Morogoro. Mtu anayetoka Kibaha kwa mfano anatoka pale Picha ya Ndege anataka kwenda Kongowe hana sababu ya kuja kwenye barabara kubwa na kuongeza foleni, anaweza tu akapita kwenye barabara hii na ikawa inaleta tija kusaidia kupunguza foleni katika barabara kubwa ambayo kwa sasa hivi ndiyo barabara kubwa ya kiuchumi inayopitisha zaidi ya asilimia 85 ya magari yote yanayoingia na kutoka Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa nataka nitoe ushauri wa Wizara, kwamba TARURA ambayo inakwenda kutoa huduma kwa wananchi na ndiyo inayotengeneza siasa ya miundombinu kwa wananchi wetu, hakika bado hawajapata fedha za kutosha. Barabara nyingi ziko katika network yao, lakini fedha ya kuhudumia barabara hizi hata katika kiwango cha changarawe zipitike muda wote bado hawanazo jambo ambalo linaifanya azma hii njema ya kumpelekea mwananchi maendeleo kwa karibu ishindwe kufanyika.

Mimi ombi langu kwa Wizara, waangalie ni namna gani TARURA itapewa fedha zaidi ili barabara hizi zote ambazo ziko katika network angalau zifike katika kiwango cha changarawe kama hazitaweza kwenda katika kiwango cha lami ili azma ya kumuhudumia mwananchi kwa karibu iweze kuwepo na waweze kunufaika sasa na hizi barabara kubwa za highway. (Makofi)

Mheshiwa Mwenyekiti, ya kwangu ni hayo machache na ninaunga mkono hoja, tuko pamoja na Wizara yetu ya Miundombinu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. SILVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti ya Wizara hii muhimu, Wizara ya Nishati ambayo kwetu na wananchi wetu ni huduma muhimu lakini ni siasa kubwa katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Wizara pamoja na watumishi wote na Mashirika yanayohusiana na Wizara hii, kwani wamekuwa wakiendelea kufanya kazi nzuri ya kutoa huduma hii kwa wananchi wetu. Katika Jimbo letu la Kibaha Mjini au Mji wa Kibaha ni Mji unaokua kwa haraka, lakini ni Mji ambao pembezoni mwa Mji huu kuna maeneo mengi ambayo bado yako katika mfumo ule wa REA na hakikia wananchi wake wengi hawawezi ku-afford kufungiwa umeme kwa ile gharama ambayo siku zote wanachaji ile ya Mjini ya kati ya shilingi laki tatu na ishirini mpaka laki tatu na Hamsini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Wizara kwa sababu siku za karibuni Waheshimiwa Wabunge tuliombwa tuainishe yale maeneo ambayo hakika hawawezi kufikia gharama hizo ili waingizwe katika utaratibu wa REA wa kulipa shilingi 27,000 na kuweza kufungiwa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wangu wa Kibaha, maeneo hayo ni pamoja na Mbwawa, Hekani, Kichangani, Kidugalo, Miomboni, Ghaza, Jerusalemu, Mtaa wa Vitendo, Zogoale, Saenii, Yonuga, Simbani, Sagale, Muheza, Mbwate, Bungo, Kokotimiza, Pumba, Galagaza, Rulanzi, Mwanaugali na Mwale vilevile Mkombozi na Lumumba. Maeneo haya tulikwisha yawasilisha REA na tayari tulikwisha ahidiwa kwamba utaratibu unafanyika ili na wenyewe waunganishwe katika ule utaratibu wa REA waweze kufungiwa umeme kwa hii gharama nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Wizara au kwa Serikali, sasa utaratibu ufanyike wa haraka kupitia bajeti hii ili wale wananchi wanaosubiri kupata huduma hii waweze kufungiwa umeme huu na wenyewe waweze kunufaika na kufurahia matunda ya kazi kubwa yanayofanywa na Mheshimiwa Rais pamoja na Wizara hii kwenda kuwapelekea wananchi umeme wa bei nafuu, kwa maana mbali na kazi za kiuchumi, mbali na kwamba umeme ni biashara lakini kimsingi kwa wananchi hawa ni huduma kubwa kwao ambayo inakwenda kuwakomboa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mradi wa kusafirisha umeme kutoka Kinyerezi hadi Arusha ule wa Msongo wa KV 400. Nafahamu Serikali ilikwishafanya jitihada ikawalipa wale wananchi ambao maeneo yao yalichukuliwa kupisha mradi huu, lakini bado kuna wananchi ambao hawajalipwa na wananchi hawa hawajalipwa kwa sababu maeneo yao yalihesabiwa chini ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha sasa malipo yalipofanyika taasisi za Serikali ziliwekwa pembeni au zilisemekana kwamba zitachelewa kulipwa wananchi walipwe kwanza, lakini kimsingi kwa maana ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuna wananchi wengi ambao maeneo yao bado yalikuwa chini ya Halmashauri kwa sababu ya kiumilikaji na hadi leo bado hawajaweza kupata fidia, kwa hiyo wamekuwa wakinung’unika wakati wenzao tayari walikwisha pata fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Wizara kwa Mheshimiwa Waziri kabla hatuja-wind up kesho, basi ningeomba Wizara itoe tamko ni namna gani hawa na wenyewe wanakwenda kupatiwa fidia ili sasa na wenyewe waweze kuwa sawa na wale wengine ambao tayari walikwishapata fidia kwa kupisha mradi huu wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba Shirika letu la TANESCO ni kubwa na linahitaji ufanisi mkubwa, tunafahamu utawala una mikakati ya kufanya transformation kubwa au mabadiliko makubwa ya kimuundo lakini kiutawala na kiutendaji. Mimi naunga mkono jambo hili kwa sababu ndiyo njia pekee ya kuendesha shirika hili kisasa, tunafahamu wazi katika kwenda kulitekeleza hili zitatokea fursa nyingi kwenda katika sekta binafsi na ndiyo mtindo wa kisasa wa kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi mahali popote Duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ombi langu kwa shirika hili au kwa Wizara, tunaomba sana wakati wanaenda kufanya mabadiliko haya kipaumbele cha kwanza au watu wa kwanza kufikiriwa ziwe ni kampuni za nyumbani kwa maana zisimamie ipasavyo local content ili makampuni ya ndani ya nchi ya wazawa waweze kupata nafasi ya kushiriki katika kazi hii au shughuli hizi kubwa zitakazotokana na mabadiliko ya kiutendaji na kiutawala ambayo yatakwenda kufanywa na shirika hili la TANESCO, ili tija ile isiishie tu kuliboresha Shirika lakini tija ile vilevile iweze kwenda kwa makampuni yetu, wananchi na hatimae kupeleka uchumi kwa wananchi wengi kama wanavyosema wenzetu waingereza kwamba tuwe na ile economical multiply effect kwenda chini kwa Watanzania wengi ambao watashirikishwa katika utaratibu huu wa kwenda kufanya transformation katika shirika letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaendelea kuipongeza Wizara hakika tulisharudi nyuma sana kwa kuacha kuchukua nafasi ya awali kwenda kujenga ile LNG plant kule Lindi. Tulianza vizuri na watu walichangamka kweli kweli, Mtwara ilichangamka, Lindi ilichangamka na hata wawekezaji wa ndani na nje walifanya kazi kubwa ya kuanza kuwekeza katika maeneo haya, lakini baadae kwa bahati mbaya tukasuasua wenzetu wa Msumbiji wakaenda mbele, lakini nina imani kwa mkakati tulionao sasa siku si nyingi mradi huu mkubwa kupita miradi mingi ambayo imekwishafanyika hapa nchini unakwenda kutimizika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali kwamba kwa kuwa tumekwishaamua tusirudi nyuma kwa maana nishati hii tayari inakwenda kuwa muhimu sana katika matumizi mbalimbali Mjini, lakini inakwenda kutuondolea adha kubwa ya kutumia nishati ambayo inatuathiri kimazingira na hususan ukataji wa miti pamoja na matumizi ya kuni na mkaa ambayo inakwenda kutuathiri katika ustawi na upatikanji wa mvua na hatimae kufanya nchi yetu ipatwe na janga la kiangazi. Kwa hiyo, ombi langu na ushauri wangu ni kwamba kwa kuwa tayari kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri tumekwisha fikia mahali pazuri basi niombe Serikali na yenyewe iendelee kuweka nguvu ili mradi huu uweze kufanyika na uweze kukamilika ili matunda yake tuweze kuyaona ndani ya nchi na hata kwenda chini kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ulikuwa ni huo na niunge mkono hoja. (Makofi)