Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Rose Kamili Sukum (6 total)

MHE. EZEKIEL M. MAIGE (K.n.y MHE. ROSE K. SUKUM) aliuliza:-
Serikali ina utaratibu wa kutoa fedha kwa ajili ya shule za bweni nchini. Kwa kipindi cha kuanzia tarehe 31/08/2013 hadi tarehe10/02/2014 Halmashauri ya Hanang ilipokea kutoka Serikali Kuu kiasi cha shilingi 508,779,500 kwa ajili ya chakula cha shule za bweni. Taarifa zinaonesha kwa fedha zilizotumika kununua chakula ni shilingi 225,585,000 kwa takwimu hizo bakaa ni shilingi 283,194,500 kwa mujibu wa Mkaguzi, bakaa hiyo haionekani kwenye account yoyote benki.
(a) Je, fedha hizo zinarudishwa Hazina bila ya kuwa na uwepo wa nyaraka zozote toka Halmashauri kuonesha muamala unavyofanya kazi?
(b) Je, kama fedha hizo hazikurudishwa Hazina nani anaweza kuidhinisha matumizi bila ya mpango wake kupitishwa na Kamati ya Fedha na Mipango ya Halmashauri?
(c) Je, kama fedha zimetumika bila kupangiwa na Kamati halali, ni kwa nini wahusika bado wanaendelea kuwa ofisini bila ya kufunguliwa mashtaka ya wizi wa kuaminika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Kamil Sukum, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014 Halmashauri ya Wilaya ya Hanang iliidhinishiwa shilingi 225,585,000 kwenye ruzuku ya uendeshaji wa shule za msingi kwa ajili ya chakula cha wanafunzi kwa shule za bweni za Katesh, Balangdalalu, Bassodesh na Gendabi. Fedha zilizotolewa zilikuwa ni shilingi 508,779,500 zikiwa ni ziada ya shilingi 283,194,500. Fedha hizo hazikurejeshwa Hazina badala yake zilibadilishwa matumizi na kutumika kwa ajili ya vifaa vya shule na ukarabati wa shule hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizo zilizoombewa kibali cha kubadili matumizi ili zitumike kununua vifaa vya shule na ukarabati wa mabweni. Hata hivyo ni kweli maombi hayo hayakujadiliwa katika Kamati ya Fedha na Mipango na kwa mantiki hiyo utekelezaji wa jambo hilo ulikiuka misingi na utaratibu wa uendeshaji wa Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na makosa hayo Mkurugenzi wa Halmashauri amesimamishwa kazi pamoja na Watumishi wengine wanne wakiwepo Afisa Mipango Wilaya, Mweka Hazina Wilaya na Wahasibu wawili ili kupisha uchunguzi. Aidha, Baraza la Madiwani limeelekeza fedha hizo zirejeshwe kupitia mapato ya ndani na tayari shilingi milioni 130 zimepelekwa kwenye akaunti ya vijiji vya Gendabi, Bassodesh, Katesh na Balangdalalu.
MHE. ROSE K. SUKUM aliuliza:-
Watanzania 89% wanategemea shughuli za kilimo na wengi wanaojihusisha na kilimo ni watu wa kipato cha chini. Serikali katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ilianzisha Benki ya Kilimo, kwa mujibu wa Mpango huo kuanzia mwaka 2011/2012 hadi 2015/2016 ilitakiwa kutoa kila mwaka shilingi bilioni 100 ili Benki hiyo iwe na mtaji wa shilingi bilioni 500; lakini hadi sasa katika kutekeleza mpango huo Serikali imepeleka shilingi bilioni 60 tu:-
(a) Je, ni lini Serikali itatekeleza matakwa ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ya kwanza katika dira ya mwaka 2025 ya shilingi bilioni 100 kila mwaka?
(b) Je, Benki hiyo ina mpango gani wa kuwafikia wakulima wadogo ambao ndio nguzo kuu nchini Tanzania katika kuondoa umasikini wa kipato?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Kamili Sukum, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Benki ya Maendeleo ya Kilimo imezunduliwa rasmi mwezi Agosti, 2014. Serikali ina nia thabiti ya kuhakikisha benki hiyo inapata mtaji wa kutosha ili kuiwezesha kutimiza lengo lililokusudiwa la kuwezesha upatikanaji wa mikopo kwa wakulima wadogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutenga fedha hatua kwa hatua na katika bajeti ya 2016/2017, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 200 ili kuiongezea benki hiyo mtaji. Katika kumaliza tatizo la mtaji, Serikali imejizatiti kuongeza mtaji huo kupitia hati fungani ya mtaji isiyo ya fedha taslimu katika maana ya (Non-Cash Bond) yenye thamani ya shilingi bilioni 800 itakayolipwa kwa kipindi cha miaka sita kuanzia mwaka ujao wa fedha wa 2017/2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kupitia ujio wa Makamu wa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) yamekuwepo mazungumzo baina ya AfDB na TADB ili kuiongezea mtaji TADB. Kwa vile mkopo huo utakopwa na Serikali, majadiliano baina ya Wizara ya Fedha na Mipango na Benki hiyo yanaendelea ambapo yatakapokamilika, yatawezesha Benki ya Kilimo kuwa na mtaji mkubwa zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Benki hii wa kuwafikia wakulima wadogo umejikita katika kuvijengea uwezo vikundi vya wakulima ili viweze kukopesheka na kuwa na uwezo wa kurejesha mikopo hiyo. Benki ya Kilimo imeanza kutoa huduma ya mikopo katika mikoa sita ikilenga kuwajengea uwezo wakulima wadogo kwa kushirikiana na Sekretarieti za Mikoa, Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, Mfuko wa Pembejeo na Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa mpango huo, Benki ilianza kwa kuvijengea uwezo vikundi 89 vya wakulima wadogo vyenye jumla ya wakulima 21,563 na kati ya hivyo, jumla ya vikundi nane vilitimiza masharti ya msingi ya kuweza kukopa. Vikundi hivyo vipo katika Mkoa wa Iringa na vina wakulima wadogo wapatao 800. Vikundi hivyo nane vimeshapata mikopo yenye thamani ya jumla ya sh. 1,006,822,010/=.
MHE. ROSE K. SUKUM aliuliza:-
Serikali hupeleka fedha kwenye Halmashauri baada
ya kupokea mpango kazi wa maendeleo au matumizi ya kawaida kwa Halmashauri husika. Kama ikitokea fedha zaidi zimepelekwa katika Halmashauri, maana yake kuna Halmashauri imepelekewa kidogo:-
(a) Je, kwa nini fedha za ziada zisirudishwe Hazina
na badala yake zinaombwa kutumiwa na Halmashauri ambayo haikuwa na mahitaji nazo?
(b) Je, Halmashauri ambazo zinakuwa zimepelekewa fedha kidogo zinafidiwa vipi ili kukidhi maombi ya mpango kazi wake?
(c) Je, kwa Halmashauri inayotumia fedha hizo
bila ya kusubiri maelekezo kama ilivyo pale inapokuwa ziada kuwekwa kwenye Akaunti ya Amana kama Memorandum ya Fedha ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa Kifungu Na. 9(2)(e) kinavyoelekeza, endapo itabainika, wanachukuliwa hatua gani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Kamili Sukum, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, upelekaji wa fedha katika Halmshauri huzingatia Mpango Kazi (Action Plan) ambao huandaliwa kwa kuzingatia bajeti iliyoidhinishwa na Bunge. Fedha hizo hupelekwa na Hazina kila robo mwaka zikiwa na maelekezo ya matumizi. Uzoefu unatuonesha Halmashauri zimekuwa zikipokea pesa pungufu ikilinganishwa na bajeti iliyoidhinishwa kwa sababu upelekaji wa fedha hizo huzingatia hali ya makusanyo kwa nchi nzima. Hata hivyo, pale inapobainika kuwa fedha zilizopokelewa zaidi ya bajeti iliyoidhinishwa na hakuna maelezo ya matumizi, ni wajibu wa Afisa Masuhuli kuuliza matumizi ya fedha hizo Hazina au Ofisi ya Rais (TAMISEMI) kabla ya kuzitumia.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza katika sehemu (a) ya jibu langu, kila Halmashauri hupelekewa fedha kulingana na bajeti iliyoidhinishwa na kwa kuzingatia mpango kazi. Fedha hupelekwa katika Halmashauri kwa kuzingatia hali ya makusanyo (Cash Budget). Kwa mantiki hiyo, hakuna utaratibu wa kufidia bajeti ambayo haikutolewa kwa mwaka husika. Mwongozo wa Bajeti huzitaka mamlaka husika kuzingatia maeneo ambayo hayakupata fedha katika vipaumbele vya bajeti inayofuata ili kupata fedha.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zote zinazotumwa katika Halmashauri huambatana na maelezo ya matumizi ya fedha hizo ambayo hupitia kwa Katibu Tawala wa Mkoa. Pale inapotokea maelezo yamechelewa kufika, ni wajibu kwa Mkurugenzi wa Halmashauri husika kufuatilia Hazina au Ofisi ya Rais (TAMISEMI) kabla ya kuzitumia. Afisa Masuhuli atakayetumia fedha za ziada bila idhini, anakiuka sheria na taratibu za fedha na anastahili kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.
MHE. ROSE K. SUKUM aliuliza:-
Serikali ina utaratibu wa kutoa fedha kwa ajili ya shule za bweni nchini. Kwa kipindi cha kuanzia tarehe 31/08/2013 hadi 10/02/2014 Halmashauri ya Hanang ilipokea kutoka Serikali Kuu kiasi cha shilingi 508,779,500 kwa ajili ya chakula cha shule za bweni. Taarifa zinaonesha kuwa fedha zilizotumika kununua chakula ni shilingi 225,585,000. Kwa takwimu hizo bakaa ni shilingi 283,194,500 na kwa mujibu wa mkaguzi, bakaa hiyo haionekani kwenye akaunti yoyote ya benki.
(a) Je, fedha hizo zinarudishwa Hazina bila ya uwepo wa nyaraka zozote toka Halmashauri kuonesha muamala unavyofanya kazi?
(b) Je, kama fedha hizo hazikurudishwa Hazina, nani anaweza kuidhinisha matumizi bila ya mpango wake kupitishwa na Kamati ya Fedha na Mipango ya Halmashauri?
(c) Je, kama fedha zimetumika bila kupangiwa na Kamati halali, ni kwa nini wahusika bado wanaendelea kuwa ofisini bila ya kufunguliwa mashtaka ya wizi wa kuaminika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA SERIKALI ZA MITAA: alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Kamil Sukum, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ ilipokea kiasi cha fedha shilingi 508,779,500 kwa ajili ya chakula cha shule za msingi nne za bweni ambazo ni Katesh, Balangdalalu, Bassodesh na Gendabi. Jumla ya shilingi milioni 225.58 zilizopangwa kwenye bajeti zilipelekwa kwenye shule za msingi za bweni kadiri fedha hivyo zilivyopokelewa kutoka Hazina. Kiasi cha shilingi milioni 283.19 zilizosalia hazikurudishwa Hazina badala yake fedha hizo zilibadilishiwa matumizi kwa kuombewa kibali cha kubadilisha matumizi kwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango kwa barua yenye kumb. Na. HANDC/ED/F.1/12/ VOL.IV/198 ya tarehe 10/04/2014 na kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa barua yenye kumb. Na. HAN/ED/F1/12/ VOL.IV/205 ya tarehe 01/08/2014.
Mheshimiwa Spika, Kamati ya Fedha na Mipango ya Halmashauri baada ya kupokea taarifa ya matumizi ya fedha, iliagiza fedha hizo zirudishwe kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya kutekeleza shughuli za ununuzi wa vifaa na samani kwa wanafunzi wa shule husika. Ili kutekeleza agizo hilo, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2015/2016, kiasi cha shilingi 130,000,000 zilipelekwa kwenye akaunti za vijiji vya Gendabi, Bassodesh, Katesh na Balangdalalu kwa ajili ya kununulia magodoro, vitanda na ukarabati wa mabweni kwa shule za msingi za bweni zilizopo kwenye vijiji hivyo. Aidha, Halmashauri imeagizwa kurejesha fedha zilizobaki kiasi cha shilingi milioni 153.19 ndani ya mwaka huu wa fedha.
Mheshimiwa Spika, kutokana na matumizi ya fedha za halmashauri yasiyoridhisha, ikiwa ni pamoja na matumizi ya fedha hizo, tangu mwezi Aprili, 2016, Mkurugenzi Mtendaji amesimamishwa kazi na mamlaka yake ya nidhamu. Aidha, watumishi wengine wanne akiwemo afisa mipango wilaya, mweka hazina wilaya na wahasibu wawili wamesimamishwa kazi na Baraza la Madiwani ili kupisha uchunguzi.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA (K.n.y. MHE. ROSE K. SUKUM) aliuliza:-

Mpango wa Serikali kupeleka fedha za afya moja kwa moja kwenye Vituo vya kutolea huduma za Afya umesaidia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na stahiki za watumishi, lakini Waganga Wafawidhi hufanya kazi za Wahasibu na Maafisa Manunuzi na hivyo kusababisha kutotoa huduma kwa wagonjwa kwa wakati:-

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kuajiri Wahasibu na Maafisa Manunuzi kwa kila Zahanati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SRIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Rose Kamil Sukum, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Mpango wa Serikali wa kupeleka fedha za afya moja kwa moja kwenye Vituo vya kutolea huduma za Afya umesaidia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na stahiki za watumishi. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali iliajiri kwa mkataba Wahasibu Wasaidizi 535 na kuwapanga katika Vituo vya Afya vya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mkataba wa kwanza kumalizika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI iliwasiliana na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na kuwaombea kibali cha ajira ambapo yalitolewa maelekezo kuwa Wahasibu Wasaidizi hawa waajiriwe na Halmashauri kwa mikataba na walipwe kwa kutumia mapato ya ndani hadi hapo Serikali itakapokuwa imewaajiri. Aidha, wahasibu hawa wana jukumu la kuhudumia Kituo husika na Zahanati zake zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haijaajiri wataalam wa manunuzi kwa kuwa manunuzi mengi katika Vituo vya Afya yanafanywa na Pharmacists ambao wapo katika Vituo vyote vya kutolea huduma ikizingatiwa kuwa asilimia kubwa ya fedha kwa Vituo hivyo ni kwa ajili ya manunuzi ya dawa, vifaa vya tiba kupitia Bohari Kuu ya Dawa ya Serikali (MSD).

Serikali itaendelea kuajiri Wahasibu Wasaidizi kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. ROSE K. SUKUM aliuliza:-

Kutokana na wingi wa watu na shughuli za kiuchumi zilizopo katika Kata ya Bassotu kama vile uchimbaji madini, uvuvi, kilimo, ufugaji na biashara na hivyo kuwa na hatari ya milipuko ya magonjwa:-

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Wodi ya Watoto, Wanawake, Wanaume na nyumba za watumishi wa Zahanati ya Bassotu?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Kamili Sukumu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kutokana na Mwongozo unaosimamia utoaji wa huduma za afya, zahanati hazina Wodi ya Watoto, Wanawake na Wanaume. Hata hivyo, kutokana na umbali uliopo kati ya zahanati hiyo na Hospitali ambao ni kilometa 55, Serikali itafanya tathmini ili kuboresha miundombinu iliyopo na kuifanya Zahanati ya Bassotu kuwa na hadhi ya Kituo cha Afya.