Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Abdallah Hamis Ulega (225 total)


MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja na ombi moja kwa Serikali. Naanza na swali, maeneo mengi nchini hususan maeneo haya niliyoyataja ya Kata ya Kala, Ninde, Wampembe na Kizumbi yanayoendeleza shughuli za kilimo wananchi wake wanaishi maisha duni. Pamoja na mkakati uliosemwa na Serikali juu ya uendelezaji wa shughuli hiyo ya uvuvi wa kisasa na ufugaji wa samaki lakini bado maeneo haya niliyotaja umaskini haupungui kwa kasi inayotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri, kwa vile na yeye mwenyewe ni mtaalam katika eneo hilo la ufugaji wa samaki, yuko tayari kututembelea katika Kata hizi nne ambazo ni maarufu sana kwa uvuvi ili kuhimiza ufugaji wa samaki na kunusuru wananchi kiuchumi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni ombi kwa Serikali. Takribani wananchi 1,000 wa Vijiji vya Kasu, Milundikwa, Kantala pamoja na Kisura wanakabiliwa na ukosefu mkubwa wa ardhi uliosababishwa na eneo lao kuchukuliwa na jeshi. Licha ya kwamba Serikali ilitoa eneo hili kwa wananchi kihalali lakini sasa hivi jeshi limetwaa eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali itume mtu au kiongozi mahsusi akauangalie mgogoro huu ili wananchi wapate mahali pa kulima kwa sababu sasa hivi wana sintofahamu kubwa sana na mvua sasa zimeanza kunyesha. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote na mimi napenda nimpongeze Mheshimiwa Mipata lakini naomba pia nichukue fursa hii kumpongeza sana na kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu mpenzi Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya mkakati mkubwa kabisa wa Serikali hii ya Awamu ya Tano ambayo inatambua kwamba jamii ya wavuvi walio wengi katika nchi yetu ni jamii maskini ndiyo maana imeamua kuirejesha Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. Huu umekuwa ndiyo mkakati mahsusi ili sasa tuweze kufika kwa wafugaji na wavuvi nchi nzima tukahamishe na kuwasimamia katika kuhakikisha kwamba wanapiga hatua ya kimaendeleo yao wenyewe kiuchumi lakini pia vilevile kupiga hatua kuwa katika mchango mahsusi kabisa wa pato la Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie kwamba sisi katika Wizara ya Mifugo na Uvuvi tuko tayari, tutakwenda Nkasi na tutafika kote katika nchi hii walipo wafugaji na wavuvi. Kauli mbiu yetu ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ufugaji ni maisha yetu, uvuvi ni maisha yetu na maisha yetu ni ufugaji na uvuvi kwa pamoja. Nakushukuru.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Kwa kuwa wananchi wengi wanahamasika na ufugaji wa samaki na kwa kuwa kuna uchache wa mbegu bora ya samaki na kusababisha samaki kutoka nje kuagizwa hasa mbegu za sato na hii inaweza kuwa hatarishi kwa samaki wetu asilia nchini. Napenda kujua Serikali inajipanga vipi kuboresha na kuwekeza katika tafiti mahsusi za uzalishaji wa mbegu bora za vifaranga wa samaki na pia kuboresha maeneo mahsusi, hizi hatcheries za uzalishaji wa vifaranga vya samaki nchini. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali inahamasisha katika ufugaji wa samaki na tunazo taasisi zetu za utafiti mathalani TAFIRI na vituo vyetu vya uzalishaji wa vifaranga vya samaki kama kile kituo chetu kilichoko pale Morogoro Kingolwira. Vituo hivi vimejipanga vyema, vina vifaranga wa kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wafugaji wote wa samaki wawe tayari sasa kuweza kwenda katika vituo vyetu vilivyopo katika zones mbalimbali, kimojawapo hiki cha zone ya Mashariki hapa Morogoro kwenda kuchukua vifaranga bora kabisa na wataweza kufanya ufugaji huu wa samaki na kujipatia kipato na lishe wao wenyewe bila wasiwasi wowote.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali moja la nyongeza. Ni ukweli usiopingika kwamba ufugaji wa samaki ni zao linaloweza kuleta matokeo ya haraka kwanza si katika tu suala la ajira lakini vilevile katika kipato cha mfugaji hata yule mwenye kipato cha chini. Hata hivyo, liko tatizo moja kubwa sana la chakula cha samaki. Taasisi nyingi zikiwemo hizi zetu za Serikali ambazo zinaonesha utafiti wa ufugaji wa samaki wanakuonesha kwamba samaki hasa aina ya tilapia anapaswa afugwe ndani ya miezi sita awe ameshafikia uzito usiopungua nusu kilo kwa kula chakula chenye formula hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza unapokuja kwenye hali halisi wale samaki wanalishwa zaidi mpaka wakati mwingine mwaka mmoja pasipokufikia uzito ule. Kutokana na hali hiyo wakulima au wafugaji wengi wanakata tamaa katika hili zoezi zima la ufugaji wa samaki. Je, Serikali sasa ina mpango gani wa kuhakikisha utafiti madhubuti unafanyika ili ile formula inayotolewa iweze kuleta tija kwa wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba udhaifu umeonekana kwa samaki wetu wanaofugwa hasa hao tilapia ambapo kutokana na chakula wanacholishwa wanachukua muda mrefu lakini ukuaji wao wa kuweza kufikia nusu kilo na sentimeta 50 ili waweze kuvuliwa umekuwa sio wenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili la ufugaji wa samaki kwa maana ya aqua culture katika nchi yetu ni jipya. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, sasa tunayo Kurugenzi mahsusi kabisa inayohusika na jambo hili la aqua culture na kupitia tafiti zetu mbalimbali za TAFIRI na vyuo vyetu vingine tunafanya jitihada za kuhakikisha tunaondoa tatizo hili la chakula cha mifugo hii ya samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wafugaji wote wa samaki nchini kwamba, baada ya muda siyo mrefu watafiti wetu hawa watabaini na kugundua lishe iliyo bora zaidi ili kuweza kukidhi mahitaji ya soko na mahitaji ya wafugaji wetu. Waendelee kujiandaa na kuendelea kuhamasishana katika ufugaji wa samaki, tatizo la chakula cha mifugo hii ya samaki litakwisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Mheshimiwa Mwenyekiti, tozo nyingi katika hizi zilizoondolewa si zile zinazomgusa moja kwa moja mvuvi. Wavuvi husasan katika Ziwa Victoria, wanasumbuliwa sana na leseni kwa mfano wanazopaswa kulipa wanapotoka Halmashauri moja kwenda Halmashauri nyingine, kuna ushuru wa uvuvi kwa mfano, na tozo nyingine za SUMATRA na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu nyingi katika hizi ziko chini ya Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003, Serikali sasa haioni sababu ya msingi kabisa kuleta sheria hii Bungeni ili Bunge liweze kuipitia na kuifanyia marekebisho?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa taarifa nilizonazo Mheshimiwa Waziri wewe ni mtaalam mbobezi kwenye eneo hili la uvuvi na unatoka kwenye eneo la wavuvi, kwa hiyo unaujua vizuri uvuvi na kwa sababu matatizo mengi ya wavuvi, hususan eneo la Ukerewe yanazungumzika, je, uko tayari sasa Mheshimiwa Waziri baada ya Bunge hili tuweze kuandamana kwenda katika Visiwa vya Ukerewe upate fursa ya kuzungumza na wavuvi na kusikiliza kero zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza anasema kwamba tozo nyingi zilizofutwa sizo zile ambazo ni kero hasa inayowasumbua wavuvi na akatuomba kuleta mabadiliko ya Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya Mwaka 2003.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie tu kwamba matakwa yake haya tunayachukua na tayari Serikali ipo katika mpango wa kuboresha moja ya Sheria ya Uvuvi ya mwaka 2003, Sheria Na. 22 na kupitia kanuni mbalimbali ambazo zitakwenda kuboresha kwa maana ya tozo hizi zilizofutwa, sawa na majibu yangu ya msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka nimhakikishie; hizi tozo, hasa ile ya movement permit iliyofutwa ilikuwa ni kero kubwa kwa wavuvi wetu na ndiyo maana Serikali hii ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Jospeh Magufuli ikaona iifutilie mbali. Na nataka nimhakikishie ya kwamba kilichobaki ni usimamizi wa kuhakikisha movement permit haiendelei kutozwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni la kwenda Ukerewe; ni kweli mimi ni mvuvi na uvuvi ni maisha yetu. Nataka nimhakikishie rafiki yangu ya kwamba tutafika Ukerewe kwenda kuzungumza na wavuvi na kwenda kuwatoa majaka roho yote yanayowasumbua. Ahsante sana.
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachukulia mfano wa mabasi, kuna utingo, kuna dereva, kuna konda, mwenye licence ya kuendesha chombo pale ni mmoja tu ambaye ni dereva, utingo hana licence wala konda. Cha ajabu katika Ziwa Tanganyika mwenye chombo anakuwa na wavuvi wake kama kumi au kumi na tano na wote wanalazimika kuwa na leseni. Je, Serikali haioni kama ni kero?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, haya ndiyo mabadiliko tunayokwenda kuyafanya katika Kanuni za Uvuvi, kuboresha ili kuweza kumuinua mvuvi wa Tanzania. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Keissy kanuni yetu ya Uvuvi tunayokwenda kuibadilisha itazingatia matakwa haya ya Waheshimiwa Wabunge.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya vijana wa Kitanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ninapenda kujua ni nini mpango wa Serikali wa kuwapatia vijana wafugaji elimu ya malisho katika ufugaji endelevu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika majibu ya Serikali kwa swali langu la msingi kipengele (b) ni dhahiri kwamba Mkoani Mwanza hakuna vikundi vya vijana/ wafugaji ambao wamejiunga na vyama hivi vya ushirika.
Je, ni lini Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa tayari kuambatana na mimi kwenda Mkoani Mwanza kukutana na maafisa vijana pamoja na maafisa ufugaji ili tuweze kutafuta namna ya kuwawezesha vijana hawa kujiunga na vyama hivyo vya ushirika?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, mpango wa Serikali ni nini wa kuwapatia elimu vijana wa nchi hii juu ya malisho.
Kwanza, kupitia mpango mkakati kabambe kwa maana ya Tanzania Livestock Masterplan ambao tunakwenda kuuzindua sasa katika eneo hili la malisho tumeweka msisitizo mkubwa sana. Nataka niwaambie vijana nchi nzima ya kwamba malisho ni uchumi, leo mbegu kilo moja ya malisho inauzwa takribani 15,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya ng’ombe mwenyewe na mazao yake, lakini uwepo wa malisho mtu ama kijana akijikita katika malisho anao uwezo na uhakika wa kupata kipato chake kitakachomsaidia katika kuendesha maisha yake. Hivyo, Serikali katika kuhakikisha hili tayari tunao mpango wa kuhakikisha mbegu za malisho zinapatikana madukani ili ziweze kuuzwa kama zinavyouzwa mbegu zingine kwa maana ya mbegu za mahindi, mpunga na nyinginezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili la Mheshimiwa Maria Kangoye ni kwenda Mwanza kukutana na kuwahamasisha vijana juu ya shughuli za ufugaji na uandaaji wa malisho; nataka nimhakikishie Mheshimiwa Kangoye niko tayari hata baada tu ya kumaliza Bunge hili kuambatana naye kuelekea Mwanza.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali na kwa jitihada ambazo wanazifanya, natambua jitihada hizo; niombe kuuliza maswali ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Ngara kuna maeneo ambapo kuna mifugo mingi zaidi kuliko maeneo haya yaliyotajwa kuwekwa miradi hii. Kwa mfano kwenye kata za Keza, Nyamagoma, Mnusagamba katika kijiji cha Mnusagamba na Ntanga. Sasa, je, Serikali iko tayari kutenga fedha kwa ajili ya kupeleka huduma hii ya malambo katika maeneo hayo kwa sababu ndiyo maeneo yenye mifugo mingi zaidi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwenye sekta hii ya mifugo, ikiwa ni pamoja na Jimbo la Ngara, hususan baada ya mifugo mingi kutoka maporini kwenye hifadhi kurudi vijijini, kuna tatizo kubwa la migogoro kwa maana ya wakulima na wafugaji, lakini Serikali iliunda Kamati kutoka kwenye Wizara sita ili kupitia mchakato kuona ni namna gani ambavyo wanaweza wakatoa suluhisho la kudumu.
Je, ni lini Kamati hii iliyoundwa ya Wizara sita itakuja na mpango au pengine ku-implement matumzi bora ya ardhi kama suluhisho la kuondoa migogoro kati ya wakulima na wafugaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Alex Gashaza, Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ameuliza juu ya lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya maeneo hayo yenye mifugo mingi. Jambo hili linapaswa yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge na wenzake katika Halmashauri waliibue na sisi Serikali tuko tayari kuhakikisha ya kwamba tunawaunga mkono ili kuweza kuondoa kero hiyo ya ukosefu wa maji kwa ajili ya mifugo katika Wilaya ya Ngara na maeneo yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ameuliza juu ya Kamati iliyoundwa na Serikali kupitia Wizara sita kuondoa matatizo ya wakulima na wafugaji, ndiyo maana nilieleza katika jibu letu la msingi ya kwamba maeneo ya Ngara yanalo tatizo kubwa la kuvamiwa na mifugo kutoka nchi jirani na ndiyo maana sisi katika Serikali tumejielekeza ya kwamba hatutarudi nyuma, tutahakikisha mifugo yote iliyotoka nchi jirani kuingia Tanzania kutufanya kuwa sisi ni eneo la malisho tutaitoa kwa namna yoyote ile ama kuikamata na kuhakikisha tunaitaifisha kwa Sheria Na. 17 ya Magonjwa ya Wanyama ya mwaka 2003. Lakini vilevile kwa sheria ya mwaka 2010 inayohusu rasilimali malisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na juu ya task force hii iliyoundwa jitihada nyingi zimeshafanyika katika maeneo haya ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba maeneo yetu ambayo tulikuwa tumeyahifadhi kama vile Mwisa II yanakwenda kugawanywa kwa ajili ya wafugaji waweze kupata maeneo ya kufanyia shughuli zao za ufugaji kwa nafasi. Naomba sasa Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wengine watupe ushirikiano kuhakikisha jambo hili linafanikiwa.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Pugu, Jimbo la Ukonga kuna Mnada wa Kimataifa wa Pugu, nimuombe Mheshimiwa Waziri kama yupo tayari tumpeleke katika eneo hili akutane na wafanyabiashara wa eneo hili ili wamueleze kero kubwa ziliyopo zikiwemo za ukosefu wa malisho na bwawa la maji na vyoo na mnada huu unaitwa wa kimataifa ambao kimsingi ndio unalisha Mkoa wa Dar es Salaam.
Mheshimiwa Waziri, upo tayari kwenda Pugu ukutane na watu hawa wakueleze kero zao kiundani zaidi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niko tayari kwenda Pugu kukutana na wafugaji hawa na wauzaji.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara imeanza kutekeleza ujenzi wa Bwawa la Mwanjolo, lakini mapungufu yaliyopo katika mkataba huo ni mabirika ya kunyweshea mifugo; je, Serikali haioni haja ya kuongeza mabirika ya kutosha ukizingatia Ukanda huo una ng’ombe wengi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sisi tunatambua ya kwamba mifugo ni maisha yetu na ufugaji ndiyo maisha yetu. Nataka nimhakikishie kwamba wao kupitia Halmashauri waibue miradi hii na sisi katika Serikali tutahakikisha kwamba tunawaunga mkono ili kusudi jambo hili linalohusu malisho na maji kwa ajili ya mifugo tatizo hili liweze kuisha.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali imefanya jitihada gani ili kuhakikisha kwamba wavuvi wanaweza kuzifikia na kunufaika na hizi fursa alizozizungumzia Mheshimiwa Naibu Waziri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha inasimamia kwa ukamilifu sekta hii ya uvuvi ili kuhakikisha inaepusha uvuvi haramu ambao utaleta uharibifu kwa mazingira?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ni jitihada gani ambazo Serikali imeshakufanya. Kama nilivyojibu katika swali la msingi ya kwamba, la kwanza, tumeendelea kuhamasisha wavuvi kujiunga katika vikundi mbalimbali ili waweze kutumia fursa zinazojitokeza, kama vile fursa niliyoitaja ya ruzuku ambapo katika mwaka huu wa 2017/2018 tumeshatenga shilingi milioni 100 ili kuweza kuendelea kuwasaidia wavuvi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Sheria ile ya Fedha ya mwaka 2007 tunaendelea kuisimamia kuhakikisha ya kwamba zana za uvuvi zinaendelea kupatikana kwa bei nafuu. Pia tunalo dirisha katika Benki yetu ya Rasilimali ambalo linahusu wakulima, wavuvi na wafugaji ili waweze kupata mikopo mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni juu ya hatua gani Serikali inachukua kukomesha uvuvi haramu ili kulinda rasilimali zetu. La kwanza kabisa Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wavuvi na jamii za wavuvi ili kulinda rasilimali zetu kwa ajili yetu na vizazi vijavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali imejishirikisha katika kufanya doria mbalimbali ambazo zimeleta matunda chanya ya kuhakikisha kwamba uvuvi haramu unapigwa vita ikiwa ni pamoja na uvuvi wa matumizi ya mabomu na uvuvi wa nyavu zisizoruhusiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho katika kupambana na uvuvi haramu, Serikali inakusudia kuleta maboresho ya Sheria yetu ya Uvuvi Namba 22 ya mwaka 2003 ili kuipa meno zaidi kuhakikisha tunaendelea kulinda rasilimali za nchi yetu. Nashukuru sana.
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na tatizo kubwa sana la wavuvi, hasa wa Kanda ya Ziwa na wa Ziwa Victoria kuchomewa nyavu zao na kusababishiwa hasara kubwa sana na Serikali. Ni lini sasa Serikali itatoa maamuzi ya kukataza nyavu hizi kutengenezwa kwenye viwanda ili wananchi wetu wasiendelee kupata hasara ya kuchomewa nyavu zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali itaendelea kutoa elimu ya kuhakikisha kwamba wananchi wanapata kujua nyavu gani ambazo haziruhusiwi na nyavu gani ambazo zinaruhusiwa.
Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kupitia sheria zetu za uvuvi tutaendelea kushirikiana na wavuvi wetu na jamii yote ya wavuvi ili kuhakikisha kwamba zile nyavu zisizoruhusiwa hatutaziacha, lakini nyavu zinazoruhusiwa ambazo zipo katika vipimo vya kisheria zitaendelea kutumika. Vilevile kuwahamasisha wawekezaji zaidi waweze kutengeneza nyavu zinazoruhusiwa kwa ajili ya kulinda mazingira yetu.
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo ya wavuvi wadogo katika Ziwa Tanganyika yanafanana sana na matatizo ya wavuvi wadogo katika Kisiwa cha Mafia. Taasisi ya Hifadhi ya Bahari Mafia imekuwa ikiwanyanyasa na kuwabambikia kesi wavuvi wadogo wa Mafia na kuwanyang’anya nyavu zao. Je, Mheshimiwa Waziri utakuwa tayari kufanya ziara Mafia na kutukutanisha sote ili kupata ufumbuzi wa tatizo hili?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie kaka yangu, Mheshimiwa Mbaraka Dau, Mbunge jirani wa Mafia ya kwamba nipo tayari kwenda nyumbani Mafia kwa ajili ya…
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kwa ajili ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Ziwa Tanganyika, Kalema, Ikola pamoja na Kapalamsenga, vijana wale wako duni sana kwa ajili ya uvuvi wa lile Ziwa Tanganyika. Je, Waziri yuko tayari kwenda na mimi ili akaone hali halisi ya vijana wale?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anna Lupembe kwamba niko tayari kwenda Ziwa Tanganyika kuonana na wavuvi wa ziwa hilo wakati wowote baada ya kumaliza shughuli za Bunge hapa.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaruhusu nyavu zisizotakiwa zinaingia nchini na Serikali hiyo hiyo inachukua kodi kwa waingizaji wa nyavu ambazo hazifai, nyavu zikishauzwa anayepata hasara ni mwananchi aliyenunua nyavu zile ambazo kumbe Serikali inafahamu hazihitajiki na ilichukua kodi. Sasa kama Serikali inaweza ikazuia madawa ya kulevya yasiingie nchini inashindwaje kuzuia nyavu zisizofaa kwa wavuvi zisiingie nchini na hivyo kuwatia hasara baada ya kuwa wameshazinunua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi jambo hili la nyavu lina mkinzano. Zipo nyavu ambazo zinaruhusiwa katika bahari lakini size hiyo hiyo ya nyavu inaweza isiruhusiwe katika maziwa yetu; wapo wafanyabiasara ambao wanaweza kuagiza nyavu kwa nia ya kusema wanazipeleka katika bahari lakini wakishafika na kuzitoa bandarini wakazipeleka kwenye maziwa pasiporuhusiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hila hii wataalam wetu na sisi kama Wizara tunaendelea kukabiliana nayo na hata sasa tunazo kesi mahakamani za jambo la namna hii. Sisi tunaomba uungwaji mkono wa kuhakikisha kwamba mkanganyiko huu tunautatua ilimradi tuhakikishe kwamba wafanyabiashara wetu, wazalishaji wetu wa nyavu, wote wanakwenda kwa matakwa ya sheria, kanuni na taratibu zetu zinazo-guide shughuli nzima hii ya uvuvi. Uvuvi ni maisha yetu, lakini ni lazima tuhakikishe tunalinda mazingira kwa ajili ya vizazi vya leo na vya kesho. Nashukuru sana.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa shamba hlili la Shishiu hakuna mifugo inayokusanywa pale na kwakuwa pia katika masterplan ya Waizara ya Mifugo wana lengo la kuzalisha mbegu na malisho kwa ajili ya mifugo ili kuweza kuboresha ufugaji wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa kuwa lengo la Wilaya ya Maswa sio kubadilisha lakini ni kuitumia kwaajili ya kuzalisha mbegu na malisho. Je, Serikali haioni umuhimu wa kufikiria upya uamuzi wake huu ili kwamba eneo hili lipewe kwa Wilaya sio kumilikisha ili waweze kutumia kwa ajili ya kuzalisha mbegu na malisho kwa ajili ya mifugo?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa pia maeneo kama haya yako mengi nchini Mheshimiwa Naibu Waziri ametaja vituo 28 pia ziko Ranchi nyingi ambazo wala hazitumiki ipasavyo; je, Serikali inaonaje ikifanya vituo hivi pamoja na Ranchi kama vituo vya kujenga uwezo wafugaji wetu ili kwamba waweze kuzalisha mbegu na malisho ambayo ni changamoto kubwa kwenye nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki, Mbunge wa Maswa Magharibi kwa swali zuri kabisa la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, umuhimu wa maeneo haya kama nilivyoeleza katika jibu la msingi bado unabaki palepale hasa ikizingatiwa ya kwamba tunakwenda katika kipindi cha Tanzania ya viwanda na eneo nyeti kabisa hili la viwanda vya uchakataji na mazao ya mifugo ndio hasa unaoangaliwa. Ninachoweza kumshauri Mheshimiwa Mashimba Ndaki yeye na wenzake katika Halmashauri ya Maswa wanaweza kuandaa mpango mkakati na wakauwasilisha katika Wizara kwa ajili ya kutazamwa kama itawezekana kuweza kuandaa hati ya maridhiano kwa maana ya memorandam of understanding kuweza kufanya haya anayoyasema ya kuboresha bila ya kubadilisha lile lengo la msingi la kutumika kwa maeneo haya kwa ajili ya mifugo na kuongeza thamani ya mifugo yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili hili la Ranch, naomba nimwambie Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki na Waheshimiwa Wabunge wote, katika masterplan yetu ambayo inaendelea kuandaliwa ni kwamba maeneo haya tunawapa umuhimu mkubwa sana na shirika letu la Ranchi za Taifa hivi sasa tuna mpango mkubwa wa kulihuisha na lina mpango mzuri wa kuhakikisha kwamba Ranchi zetu zinakwenda kusaidia kuinua tasnia hii ya huduma za mifugo na hatimaye kuleta kipato kikubwa kwa nchi yetu. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kutokana na jibu la msingi alilojibu Mheshimiwa Waziri ni kwamba ranchi ile imepewa wawekezaji wazawa, ni kweli; lakini wao wazawa wanawakodisha wananchi kulima na si kama vile mkataba unavyosema. Hiyo ni moja.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, mkataba ni mkataba unaweza ukavunjwa kama unakiukwa. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuvunja huo mkataba na kuwapatia wananchi wafugaji wa Mbarali waweze kufuga kwani hawana nafasi za kufuga kutokana na maeneo tengefu kuzuiwa na Serikali? Naomba Serikali iwapatie wananchi waweze kufuga mifugo yao. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ni juu ya wawekezaji wanavunja mkataba kwa kuwakodisha wananchi. Jambo hili tumelisikia na ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumeweka mkakati kwanza kabisa tunathaminisha Ranchi zetu zote katika Taifa letu kwa kuangalia ile mikataba yote ambayo tuliwakodisha wawekezaji ambao hawakukidhi mahitaji yetu sawa na mikataba; tutavunja kwa kutangaza upya na kuwakaribisha wafugaji wote wenye uwezo wa kuweza kufuga kulingana na matakwa ya mkataba.
Mheshimiwa Spika, lakini la pili, Mheshimiwa Mwakagenda anauliza kama tutawapa wananchi. Lengo letu sisi ni kuona kwamba ranchi hizi zinatumika kwa malengo mahususi; mosi ya kuhakikisha pia hata ranchi hizi zitusaidie katika kupunguza migogoro ya wafugaji na wakulima; lakini mbili, ranchi hizi ambazo zimetapakaa nzima, ziwe ni sababu kubwa ya kuongeza kipato katika Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, huu mkakati utakapokamilika na tutakapokuja nao; tunaomba Wabunge wote nchi nzima watupe ushirikiano ili tuweze kufanikisha ajenda hii ya kusukuma mbele tasnia ya ufugaji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, uvuvi wa bahari Kuu unahitaji uwekezaji wa fedha na mitaji na wavuvi wengi katika maeneo ya Ukanda wa Pwani walikuwa wanatumia uvuvi wa kupiga mabomu ili kupata samaki na Jimboni kwangu katika maeneo ya Mchinga, Ruvu, Mvuleni, Maloo na maeneo mengine wale watu wameacha sasa upigaji wa mabomu kwa kufuata na kutii sheria za nchi sasa.
Je, nauliza Serikali ina mpango gani ya kuwasaidia hawa wavuvi ambao walikuwa wanavua kwenye eneo la bahari kuu kwa kutumia mabomu na sasa wameacha kwa kutii sheria wana mpango gani wa ziada wa kuwasaidia ili waendelee kuvua?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ukanda wetu wa bahari una takribani urefu wa kilometa 1,424 kutoka Tanga mpaka Mtwara, lakini ukiacha maeneo ya Miji Mikuu kama Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, maeneo yote yaliyopo kwenye ukanda wa bahari watu wake ni maskini sana. Nataka kujua, Serikali inajifunza nini kwa watu wa Ukanda wa Pwani kuwa maskini kwa kiwango kile wakati wana rasilimali hii nzuri ya bahari? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UVUVI NA MIFUGO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ametaka kujua mikakati zaidi ya namna ambavyo Serikali imejipanga kuwasaidia wavuvi ili waweze kuvua katika eneo la bahari kuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi ya kwamba Serikali ina mipango kadha wa kadha na tayari tumekwisha anza nayo. La kwanza ni hili la kuwawezesha kupata ruzuku kupitia vikundi vyao ambapo wavuvi mbalimbali katika nchi yetu wamepata ruzuku hii ya mashine. Hata yeye Mheshimiwa Bobali wavuvi wake wa jimbo la Mchinga tuko tayari kuhakikisha kwamba wanapata mashine hizo za kuweza kwenda kuwasaidia kwenda kufika bahari kuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama haitoshi, Serikali kupitia Taasisi mbalimbali na mifumo ya ushirikiano tunao mradi mkubwa wa SEOFISH ambao utakwenda kuhakikisha kwamba kama tulivyofanikiwa katika Mradi wa MACEMP hapo nyuma utakwenda kuwasaidia wavuvi hawa wa Ukanda wa Pwani kuweza kupata elimu za ujasiriamali, kuweza kuwasaidia kivyombo na kimifumo ili waweze kuwaondoa katika umaskini.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili linahusu kwa nini na Serikali ina mpango gani. Ni kweli jamii nyingi za wavuvi wakiwemo wavuvi wa Jimbo la Mkuranga katika eneo la Kisiju ni kweli wapo katika hali ya umaskini na wavuvi wengine wote nchini. Ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tano ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kujua hilo tukadhamiria kuona kwamba tuondoe tozo mbalimbali ambazo zinawagusa wavuvi na kuwarudisha nyuma na kupata unafuu wa maisha yao. Tutaendelea na jitihada hizo ili kuhakikisha wavuvi wetu wanapiga hatua ya maendeleo. (Makofi)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Sambamba na swali la msingi la Mheshimiwa Bobali napenda niulize swali langu la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tunafahamu kwamba kwenye ukanda wa Pwani wavuvi wake ni maskini sana hasa katika mikoa hiyo iliyotajwa na ninataka nizungumzie Mkoa wa Lindi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Lindi hauna viwanda, rasilimali pekee iliyopo ni ya bahari na wavuvi wanategemea bahari hiyo ili kujipatia riziki zao. Wavuvi hao wote kule wanavua samaki wengi sana matokeo yake baada ya kuvua samaki wale kwa kuwa wanakosa soko kinachofanyika, samaki wale ni kuwakausha kwa mazingira ya kwetu tunaita ng’onda. Samaki wale wanafanywa kuwa ng’onda yaani samaki wakavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaamini kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ya viwanda. Je, Serikali ina mpango gani juu ya kutuletea au ya kuhakikisha kwamba wavuvi wale wanatengenezewa viwanda ili kuondokana na umaskini waliokuwa nao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, Lindi sasa ni ya viwanda na ushahidi upo tayari wa kutosha kutokana na malighafi hiyo ya upatikanaji wa gesi. Lindi inanukia katika viwanda na tayari maeneo kama ya Kilwa yameonesha mfano, kuna kiwanda kikubwa sana cha mbolea ambacho kinaenda kujengwa pale. Nina imani kwa uwepo wa malighafi hii ya samaki na nina imani kwa kuwa Serikali yetu ya Awamu ya Tano ni Serikali ya viwanda na kwa kuwa Mheshimiwa Mwijage na Wizara yake wanafanya kazi kubwa sana ya kuhamasisha viwanda viweze kujengwa na sekta binafsi, ninaamini wawekezaji watavutika na wataenda kuweka kiwanda cha uchakataji wa samaki katika eneo la Lindi na kuondoa kilio hiki cha kukosekana kwa kiwanda cha samaki katika mwambao wetu huu wa Pwani. (Makofi)
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miaka kumi mfululizo ulimwenguni sekta inayokua kwa kasi katika sekta ya kilimo ni sekta ya samaki. Serikali ipo tayari sasa kuwasaidia wavuvi walioko Ukanda wa Pwani kuondokana na umaskini kwa sababu sekta hii imeonekana ni sekta inayokua kwa kasi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iko tayari kuwasaidia wavuvi kusonga mbele.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Na mimi naomba nimuulize Naibu Waziri swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa Ziwa Tanganyika kulikuwa na uharamia, wale wavuvi walikuwa wakivamiwa na maharamia kutoka nchi za jirani na kuwapokonya nyavu zao na hata mitumbwi yao. Je, Serikali imedhibiti vipi maharamia hawa katika Ziwa Tanganyika?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba wavuvi wetu wa Ziwa Tanganyika na hata wavuvi katika Ziwa Victoria wamekuwa wakivamiwa na maharamia.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie kwamba Serikali imepata taarifa hizi na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vimejipanga ipasavyo kuhakikisha wavuvi wetu wanalindwa ili waweze kufanya shughuli zao za uvuvi kama kawaida bila ya hofu yoyote.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imejikita kwenye kutoa misaada midogomidogo kwa wavuvi kama vile engine na nyuzi za kushonea nyavu za wavuvi. Je, Serikali iko tayari kuwakopesha wavuvi wa Kilwa zana za kisasa kama vile boti kwa ajili ya vikundi hivyo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, Serikali au majibu ya Waziri yameshindwa kuthibitisha kama yamewasaidia wavuvi wa Kilwa kupata zana hizo za kisasa na inawezekana kabisa wavuvi wa Kilwa hawana taarifa yoyote kuhusiana na utaratibu huu. Sasa Serikali au Waziri anaweza kunithibitishia kwamba katika hizo mashine zilizobaki wavuvi wa Kilwa wanakopeshwa mashine hizo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ipo tayari kuwawezesha wavuvi wa Kilwa? Ndiyo, Serikali ipo tayari kuwawezesha wavuvi wa Kilwa kupitia vikundi vyao. Tena na hapa naomba nimuelekeze tu kwamba vikundi hivyo vinaweza vikatumika hata vile vya BMU (Beach Management Unit) na mashine hizi bado zipo, tunawakaribisha Waheshimiwa Wabunge wote ambao watahitaji mashine hizi wafuate utaratibu kupitia kwa Maafisa Uvuvi wetu ambapo watapeleka kwa Mkurugenzi na baadae maombi yale yatafika Wizarani katika Idara yetu ya Mafunzo na Elimu ya FETA kwa ajili ya kuweza kuwapatia wavuvi wetu ili waweze kufanya uvuvi wenye tija.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri, pamoja na mikakati mizuri ya Serikali katika kusaidia wavuvi kuwawezesha kwa namna mbalimbali kwa mikopo na vifaa, kwa Kanda ya Ziwa na Ziwa Victoria kwa sasa hali imekuwa tofauti. Hivi tunavyozungumza wananchi wavuvi wa Kanda ya Ziwa, Mikoa ya Ziwa Victoria wanapata taabu kutokana na zana zao, nyavu, mitumbwi kuchomwa moto na faini zisizokuwa rafiki kwa maisha yao halisi na kazi wanayoifanya.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kupambana na suala hili la uvuvi haramu kutokufika kwenye kiwango cha kumuumiza mvuvi ambaye tunataka tumsaidie afike mbali zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na mipango yake ya kuhakikisha kwamba inawawezesha wavuvi wadogo wadogo kote nchini ikiwemo wavuvi wa Ziwa Victoria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mabula amezungumzia juu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha tunapambana na uvuvi haramu. Ni kweli Serikali inaendelea na kazi ya kupambana na uvuvi haramu kwa kuzingatia Sheria ya Uvuvi Namba 22 ya mwaka 2014 na Kanuni yake ya mwaka 2009 ambayo kwa pamoja na Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 tumeendelea kuhakikisha kwamba tunafanya kazi kubwa ya kudhibiti uvuvi haramu kwa ajili ya ulinzi wa rasilimali za nchi yetu. Naomba niwahakikishie wavuvi wa Kanda ya Ziwa kwamba zoezi hili ni kwa manufaa ya Taifa letu na vizazi vyetu vya leo na vya miaka ijayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu nyavu mbalimbali ambazo anazisema Mheshimiwa Mabula, tayari tumepata maombi ya kutoka kwa wadau mbalimbali ya kuhakikisha kwamba wanaagiza nyavu zilizo na viwango kwa mujibu wa sheria ili ziweze kusambazwa katika maduka ili wananchi wa kule Kanda ya Ziwa waweze kununua na kuweza kuendelea na shughuli zao za uvuvi bila ya kuvunja sheria.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko la mahitaji ya samaki limekuwa kubwa sana kwa sababu idadi ya Watanzania imekuwa na hata watoto wangu Wasukuma sasa wanajua utamu wa samaki wa baharini.
Mheshimiwa Waziri tatizo sio nyavu, sio ndoana wala sio nyuzi bali ni namna ya kuwafikia wale samaki, uvuvi wa kisasa unahitaji kuwa na gas cylinders na mask na vitu kama hivyo uzamie ufike kule, samaki sasa wanapatikana katika kina kikubwa cha maji. Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kwa wavuvi wetu na vifaa vya kisasa ambavyo vitawasaidia wavuvi wetu kuweza kuwafikia samaki huko waliko na sio nyavu, nyuzi na ndoana?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa swali la nyongeza la Mheshimiwa Salim alilouliza kwamba Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wavuvi hawa kuweza kupata fursa ya kwenda katika maeneo yenye samaki kwa urahisi. Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika hatua za awali za kuhakikisha kwamba tunakwenda sambamba na ongezeko la mahitaji ya samaki, tumeingia mkataba na nchi ya Maldives ambapo hivi sasa tunakwenda katika kuboresha teknolojia yetu. Mvuvi anapotoka mwaloni au anapotoka pwani anapokwenda kuvua tayari patakuwa na vyombo vya satellite katika vituo rasmi kumwezesha kujua wapi samaki waliko kwa maana ya distance gani katika eneo la bahari au la ziwa. Teknolojia hii itamsaidia anapotoka pale kuwa na uhakika kwamba atakapokwenda pale atapata mazao hayo ya bahari na maziwa kwa urahisi na itamsaidia kutumia rasilimali kidogo ya mafuta na muda mchache lakini akiwa amepata mazao ya kutosha.
MHE. KABWE Z.R. ZITTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunavyozungumza wavuvi wa Kanda ya Ziwa hasa Soko la Mwaloni Mwanza hawana uwezo wa kuuza mazao yao ya samaki popote pale Tanzania. Akitaka kupeleka Mtwara, Kigoma, Morogoro, Dodoma, Serikali inamtaka alipe export royalty pale Mwanza kwa mazao ambayo anayauza ndani ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Wizara ya Mifugo na Uvuvi inanyanyasa wavuvi wa Kanda ya Ziwa na sasa nasikia kwamba wataelekea mpaka wavuvi wa Kigoma na Mbeya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii ya Awamu ya Tano, haina nia ya kumnyanyasa mvuvi wa Tanzania. Nia yetu ni katika kuhakikisha kwamba mosi, tunalinda rasilimali za nchi yetu. Tunahakikisha kwamba mianya yote ya upotevu wa mapato yatokanayo na rasilimali za nchi yetu, ni lazima tudhibiti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti wetu umetuonesha, anayoyasema Mheshimiwa Zitto ni mazao ya samaki kule Kanda ya Ziwa maarufu kama kayabo. Utafiti wetu kayabo kwa kiasi kikubwa haziliwi Tanzania, Kanda ya Ziwa yote hakuna walaji wakubwa wa kayabo. Imethibitishika kupitia tafiti zetu kayabo inaliwa zaidi nje ya mipaka ya nchi yetu na kwa kiasi kidogo sana katika Mikoa ya pembezoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi nia yetu sio kuwanyima wafanyabiashara na wadau wa uvuvi kufanya shughuli za uvuvi bali ni kuhakikisha mapato yetu hayawezi kupotea. Ndiyo maana tumewaomba wahakikishe kwamba wanalipia export royalty kwa sababu tulikwenda katika mipaka ya Ngara na kwingineko ambapo wananchi wenyewe kwa utafiti mdogo tulioufanya wametuthibitishia kwamba pale Ngara mathalani ulaji wa kayabo ni mdogo sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, samaki wale wengi wanakwenda nje ya mipaka yetu. Wavuvi wale na wafanyabiashara wasio kuwa na nia njema na mapato ya nchi yetu wanatumia fursa hiyo kudanganya kwamba wanapeleka Ngara, Songwe Tunduma na kwingineko mipakani mwetu, hali ikiwa si hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wote tuungane mkono katika wakati huu ambapo tunajaribu kuhakikisha kwamba rasilimali za nchi yetu zinainufaisha nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa samaki mchango wake kwa Wizara, Halmashauri na Serikali Kuu haizidi shilingi bilioni 10 kwa mwaka, sisi tunataka tutoke katika shilingi bilioni 10 twende kwenye shilingi bilioni 200. Uwezo huo tunao, sababu hizo tunazo, tunaomba mtuunge mkono ili tuweze kufika mahala hapo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOYCE B. SOKOMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli inasikitisha kwa Mheshimiwa Naibu Waziri kuleta majibu ambayo hayaridhishi.
Kwanza ni uongo, kokolo la milimita 10 linavua dagaa na wale sangara wadogo ina maana kwamba unapowavua unaenda kuwatupa? Naomba muwe mnakaa mnaleta majibu ambayo ni ya uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninakwenda kwenye maswali yangu ya kimsingi. Ziwa Victoria kuna samaki ambao nature yao ni wadogo, kwa mfano furu, gogogo pamoja nembe. Wizara inatenganisha vipi uvuvi huu wa samaki wa aina ya gogogo na sangara? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Ziwa Victoria linatumika na nchi tatu ambayo ni Kenya, Uganda na Tanzania yenyewe; na ndani ya ziwa hakuna ukuta ambao utatenganisha samaki kutoka Tanzania kwenda Uganda au kwenda Kenya, je, Serikali inafahamu kwamba wavuvi wa Tanzania wanapata shida kulinganisha kuliko wavuvi wa Kenya na Uganda? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza nataka nimthibitishie kwamba nyavu za kuvua dagaa za milimita nane zipo kwa mujibu wa Sheria Namba 22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 kanuni namba 58 (1) (a)ukienda kusoma utakuta pale size ya milimita nane kwa ajili ya dagaa wa maji baridi na milimita 10 section hiyo hiyo 58 (1)(b) utakwenda kukuta kwa ajili ya milimita 10 zile za baharini, kwa hivyo si uongo ni mambo ya ukweli.
Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa upande wa sangara wadogo anaowazungumzia, ni kweli nyavu hizi za milimita nane zitakapokwenda katika ziwa hazitachagua, tunafahamu hilo jambo. Kwa vyovyote vile sangara wadogowadogo ama sato watavuliwa na hiyo kwa kitaalamu tunaita bycatch kwa maana ya kwamba wale ambao hatukuwatarajia kanuni zetu na sheria zetu ziko wazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mvuvi wa dagaa kama atakwenda kuvua kilo 100 atayoipata kwa ajili ya dagaa kwa vyovyote vile anaweza pia kwenda kupata kiasi cha kuanzia kilo moja hadi kilo 10 ya samaki ambao hawakutarajiwa na hivyo tunafahamu jambo la namna hiyo wala sio jambo geni kwamba samaki anaweza akaenda akanaswa katika mtego ambao si wa kwake.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la lake la pili sasa Mheshimiwa Sokombi ni kuhusuiana na jambo la kuwatesa wavuvi wetu wa Tanzania na wavuvi wa nchi jirani, kwa maana Ziwa Victoria hili ni mali ya nchi tatu sisi Waganda na Wakenya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nilihakikishie Bunge lako kwamba tayari nchi ambazo tuna-share nao Ziwa Victoria wametuletea maombi, na mijadala inaendelea ya kuweza kushirikiana katika ulinzi shirikishi wa Ziwa letu Victoria na module ambayo wao inawavutia sana ni module hii ambayo sisi Watanzania tunaitumia.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli samaki kama sangara ni samaki wanaosafiri umbali mrefu, lakini nataka nikuhakikishie bado fursa kubwa ya uvuvi katika Ziwa Victoria kwa upande wa Tanzania ambao ndio tunamiliki sehemu kubwa ipo kubwa na wavuvi wamekuwa wakinufaika na sisi wenyewe kama nchi tumekuwa tukinufaika.
Naomba Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kwa ujumla wake wajue kwamba Ziwa Victoria hili ni mali yetu, ni mgodi wetu, tuulinde kwa ajili ya kizazi chetu cha leo na kizazi kijacho. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali lakini pia nashukuru kwa kuchukua ushauri wangu. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mkakati wa kufikia uchumi wa viwanda unalenga pamoja na mambo mengine kutatua changamoto ya ajira hususan kwa vijana, na kwa kuwa viwanda vya ngozi nchini vinakabiliwa na changamoto ya kodi kubwa katika malighafi ya kuchakata ngozi.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa tax incentives kwa viwanda vinavyozalisha mazao yanayotokana na mifugo ili kufikia malengo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, Serikali haioni haja ya kuwa na breeding program ili kuongeza kiwango na ubora wa mazao yanayotokana na mifugo Tanzania. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako naomba sasa nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba na naomba nimpongeze sana kwa maswali yake mazuri yanayolenga katika kuhakikisha kwamba Tanzania ya viwanda inapatikana lakini pia tunazalisha ajira kupitia sekta yetu muhimu ya mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza linaeleza juu ya suala la kufanya mkakati au Serikali ina mkakati gani wa kuweza kuvipendelea viwanda vyetu vya ndani katika tasnia ya ngozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yetu tayari imeshapeleka mapendekezo Wizara ya Fedha ya kuhakikisha kwamba kodi zote zinazotozwa katika accessories za uchakataji wa ngozi ziweze kupunguzwa ama kuondolewa kabisa ili kusudi kuweza kuhamasisha uwekezaji zaidi kwenye tasnia hii ya ngozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo tumehakikisha tunapendekeza Wizara ya Fedha iweze kuongeza viwango kwa bidhaa za ngozi zinazotoka nje ya nchi kuingia nchini hasa za mitumba ili kusudi kuweza ku- discourage uagizaji wa bidhaa hizo na uwekezaji zaidi ufanyike ndani ya nchi yetu, na huu ndio mtazamo wetu kama Wizara ya Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili linahusu mpango mkakati wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wa kuweza kupata mifugo bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mpango wa kuhamasisha, tunaita artificial insemination au uhimilishaji wa mifugo yetu na hii tumefanya kwa kuanzisha vituo maeneo mbalimbali takriban vituo sita katika nchi, na tunacho kituo kikubwa sana pale Arusha cha NAIC pale Usa River ambacho kinazalisha mbegu bora. Vilevile zile mbegu zinatawanywa katika hivyo vituo vingine vilivyopo kote nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na mkakati huo tumekuwa tukinunua mbegu bora hata kutoka nje ilikuweza kuja kuongeza ubora wa mifugo yetu tuliyonayo hapa nchini. Vilevile tunakwenda katika kuhakikisha kwamba tunaboresha sheria yetu ya mbali za mifugo ili kusudi kuweza kwenda sambamba na mabadiliko hayo tunayoyataka ya kuboresha mifugo yetu hapa nchini ili tuweze kupata nyama bora na tuweze kupata maziwa bora na kwa wingi, ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nilipenda tu niongezee, kwanza nilitaka nithibitishe kwamba mapendekezo yaliyotoka Wizara ya Mifugo ni kweli yamefika Wizara ya Fedha na hapa mkononi mwangu nina bangokitita lina kurasa 53 ya mapendekezo ya maboresho ya kodi mbalimbali zikiwemo hizi za tasnia ya mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Zainab avute subira kidogo Serikali itaji- pronounce kupitia hotuba kuu ya Serikali. Nimuhakikishie kwamba kabisa ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba viwanda vyetu vya ndani vinapewa ahueni ya kodi mbalimbali kadri itakavyowezekana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa nioneshe masikitiko yangu na kwa namna gani Serikali haiwezi kuweka kumbukumbu. Mwaka 2016 niliuliza swali hili na majibu walinipa haya haya licha ya kwamba aliyekuwa Waziri alikuja Tarime na akajionea hali halisi na akatoa agizo kwamba ule mnada ufunguliwe, lakini leo mnaleta majibu ya kumbukumbu za mwaka 1997. Maswali yangu mawili ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wafanyabiashara wa ng’ombe wanapeleka ng’ombe nchini Kenya kwa mnada ambao upo mpakani wa Mabera kupelekea upotevu mkubwa wa mapato ambayo yangekuja Tanzania kupitia multiplier effect, Wakenya wangekuja kununua zile ng’ombe Tanzania kwa sababu wanategemea ng’ombe za kutoka Tanzania kuliko ilivyo sasa hivi.
Mheshimiwa Spika, ni kwa nini Serikali hamkutaka kutumia rejea ya muhtasari ya kikao cha mwaka 2016 ambapo tulikaa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Tarime, Waziri na watendaji wa Wizara husika pamoja na mimi Mbunge na baadaye tukaongea na wananchi? Kwa nini hamkutumia ule muhtasari ili mweze kufuata maamuzi yaliyofikiwa kuweza kufungua Mnada wa Magena?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, wafanyabiashara wa ng’ombe ambao wanapeleka Kenya wamekuwa wakipata usumbufu mkubwa sana kwenye kuvusha ng’ombe hizi. Kwa kuwa mnada ambao wameuweka rejea wa check point ya Kirumi hautoi suluhishi, kwa sababu wakinunua ule mnada siyo wa mpakani wanapokuja kuvusha ng’ombe kwenda Kenya wanasumbuliwa sana.
Ni kwa nini sasa Waziri (maana yake inaonekana hamtunzi kumbukumbu) husika usije tena kwenye Mnada wa Magena uweze kujionea uhalisia na maamuzi yale ili sasa uweze kuruhusu mnada huu kufunguliwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko na kwa hakika Mheshimiwa Esther Matiko anashiriki kikamilifu katika kumuunga mkono Mheshimiwa Rais juu ya ulinzi wa rasilimali za nchi yetu na ndiyo maana anasisitiza sana kuhakikisha rasilimali za mifugo zinaweza kudhibitiwa pale ili ziweze kuinufaisha nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza anatusisitiza kwa nini tusitumie Mnada wa Magena sawa na muhtasari wa mwaka 2016 ilipokaa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya kule
Mara na Wizara yetu; na swali la pili, kwa nini Mheshimiwa Waziri asiende Magena?
Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie kwamba hivi sasa Wizara yetu imeunda tume maalum ambayo inapitia maeneo yote katika nchi yetu kufanya tathmini ya minada tuliyonayo ya awali zaidi ya 480 na minada ya upili na mipakani ili kuweza kujiridhisha na maombi yaliyoletwa. Nataka nimwambie kwamba moja ya eneo ambalo tutalifanyia kazi baada ya tathmini hii inayokwenda kukamilishwa na Wizara na wataalam wetu, ni hili alilolileta hapa Mheshimiwa Esther Matiko.
Mheshimiwa Spika, kwa kumhakikishia ni kwamba tutafika Magena pia. Mimi kama Naibu Waziri na Waziri wangu tutakubaliana, tutakwenda Magena kujiridhisha na hiki anachokisema. Kwa faida ya nchi yetu, tukiona kwamba jambo hili lina faida nasi, tutalitekeleza sawa na ushauri wake. Ahsante. (Makofi)
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, kwa masikitiko makubwa niiombe Serikali inapokuwa haina majibu ya maswali tunayouliza basi wasitujibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili nilichangia bajeti 2015/2016 Naibu Waziri akiwa Olenasha yule pale akanijibu kwamba hivi ni vifaranga vya mfano milioni 21 ndio vimezalishwa kwa ajili ya kuwapelekea wakulima imo katika kitabu cha bajeti cha Wizara hii 2015/2016; leo Serikali inaniambia kutoka 2009/2010 mpaka 2017/2018 imezalisha vifaranga milioni 21 na kuvigawa. Tukisema Mheshimiwa Jenista anakuja juu ni uongo uliotukuka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali haina majibu isitujibu kwa sababu tunafuatilia haya mambo.

Sasa mimi siwezi kukubali kama Serikali imezalisha ina mpango huu swali la kwanza ninalomuuliza Mheshimiwa hata siku hiyo katika mjadala wangu niliuliza hivi vifaranga miloni 21 kwa Tanzania kwa mwaka vinatosha hata mboga ya siku moja kwa Watanzania maana hata shemeji zangu wamasahi wanakula samaki Je, Serikali iko serious kweli? Kwa hiyo Je, vinatosha hata hizo tani 50 mnazosema ikifika 21 zinatosha hata kwa mboga ya siku moja? Wako serious hawa kweli? Swali la kwanza hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, katika bahari sasa kuna upungufu mkubwa wa samaki baharini na ongezeko la walaji wa samaki limeongezeka, je, kule baharini mna mpango gani wa kuongeza uzalishaji wa vifaranga vya samaki? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote na Watanzania; Wizara yetu ina nia thabiti ya kuhakikisha kwamba ufugaji wa samaki na kusambaza vifaranga kwa watu ni jambo ambalo linapewa kipaumbele. Mheshimiwa Mbunge ana wasiwasi na takwimu tulizozitaja zinazohusu usambazwaji wa vifaranga milioni 21 nilivyovitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie kwamba katika vituo vyetu nilivyovitaja, Kingolwira pale Morogoro ninao uhakika wa kwamba vifaranga hivyo vinazalishwa na vipo kwa ajili ya wakulima wetu na wafugaji wetu. Kama ana taarifa tofauti na hiyo sisi Wizara yetu ipo tayari kupokea taarifa yake iliyo tofauti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka nimwambie kwamba katika kuhakikisha kwamba ufugaji wa samaki unapewa kipaumbele Serikali tumehakikisha katika msimu huu tunaokwenda nao wa fedha wa 2018/2019 tunaendelea na mazungumzo ya Wizara ya Fedha ili kuhakikisha tozo na kodi mbalimbali ambazo zinazuia ama kurejesha nyuma sekta hii ya ufugaji wa samaki zinaondolewa kusudi Watanzania walio wengi waweze kufuga samaki, waweze kupata kipato, waweze kupata lishe na tuache biashara ya kuagiza samaki kutoka nchi za nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge katika swali lake la pili ametaka takwimu ya kwamba je, hii tani 50 niliyoitaja ndiyo inayotosheleza? Ni kwamba hivi sasa katika nchi uwezo wetu wa kuzalisha samaki ni tani 350,000 kwa mwaka, ambapo tani zaidi la 250,000 zinatoka katika Ziwa Victoria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hitaji la samaki katika nchi ni tani 700,000 kwa hiyo tuna gap ya tani 350,000 na ndiyo maana ni muhimu sana katika aquaculture katika kipindi hiki kuliko kipindi kingine chochote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameniuliza tuna mipango gani na bahari yetu. Mpango tulionao hivi sasa katika uzalishaji wa samaki kwenye bahari tuna kitu tunaita cage farming. Cage farming ni uzalishaji wa samaki wa kufugwa katika bahari, katika mito na katika maziwa. Mkakati huo tumeuanza na unakwenda vizuri. Tumeshaweka cage za kutosha pale Bagamoyo, zaidi ya cage 40. Tunaendelea kuweka cage vilevile katika Ziwa Victoria na maziwa yetu mengine ili kuhakikisha kwamba ufugaji wa samaki na kuzifikia hizi tani 50,000 unapatikana. Nawahamasisha Waheshimiwa Wabunge wote ya kwamba ufugaji wa samaki unalipa, na wewe Mheshimiwa Salim ingia katika ufugaji wa samaki uweze kunusurika pia vile vile katika kuinua kipato chako. Ahsante.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, ningependa kupata majibu ya Serikali, kwa nini sekta hii ya uvuvi nchini iko nyuma sana au haikui kabisa ukilinganisha tu na nchi jirani zetu za Kenya na Uganda ilhali sisi tuna maeneo makubwa zaidi ya rasilimali maji nchini na wavuvi wengi wa kutosha. Sasa kwa nini tunasababisha kwamba sekta hii ya uvuvi iko chini sana kiasi ambacho tunaagiza samaki kutoka nje wakati rasilimali tunazo, wavuvi tunao, ili kukuza uchumi wa hawa wavuvi husika pamoja na uchumi wa nchi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa swali zuri sana la mwalimu wangu Dkt. Semesi Sware. Anauliza ni kwa nini sekta ya aquaculture (ufugaji wa samaki) bado iko chini Tanzania ukilinganisha na nchi jirani za Kenya na Uganda. Ni kweli, Uganda wanazalisha tani za samaki zisizopungua 30,000 na Kenya wanazalisha tani zisizopungua 25,000, sisi tuko chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waganda waliweka mkakati mzuri wa cage farming na uzalishaji wa kambale, lakini vilevile Wakenya waliweka mkakati mzuri wa kuhakikisha kwamba Serikali yao inapeleka nguvu ya kutosha katika county zote nchini kwao ili kuhakikisha wanajenga vizimba na mabwawa mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Sware na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba mkakati wa Wizara yetu ya Mifugo na uvuvi tunataka tufike mahali huko. Nataka niwahakikishie ya kwamba tayari tumeanza kazi hiyo. Idara yetu ya Aquaculture zipo sheria ambazo zilikuwa zinasababisha tusiende mbele kama nilivyotangulia kusema katika jibu langu la msingi; ambazo tayari tunakwenda kuzifanyia marekebisho. Ninaamini baada ya kufanya mabadiliko hayo yote, na kwa mkakati ambao tunao kama Wizara tutatoka na kwenda mbali sana katika sekta hii ya uzalishaji ya aquaculture. Ninashukuru sana. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Waziri anajibu swali hapo amezungumza kwamba upo mkakati wa kuzishirikisha Halmashauri na kuweza kuingia katika uzalishaji huu wa samaki.
Sasa kwa bahati mbaya sana mimi natokea katika Milima ya Usambara ambako huko hakuna mito, hakuna mabwawa, hakuna chochote, sisi samaki tunamuona kwenye picha na wenzangu Wapare kule Same. Sasa anatuambia nini, Wizara ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba hizi Halmashauri ambazo hazina mito wala maziwa zinafaidika na huu uzalishaji wa samaki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii ya kumjibu Mheshimiwa Shangazi swali lake la nyongeza na anauliza Wizara ina mkakati gani wa kuwasaidia watu wa milimani ambao hawana maziwa, hawana mabwawa wala hawana maji yanayotiririka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mpango mzuri sana na hivyo nampongeza sana Mheshimiwa Shangazi na ni ukweli kwamba samaki ni chanzo cha protein, lakini vilevile na madini yaliyo muhimu kabisa katika mwili wa binadamu yanayoenda kuimarisha mifumo ya mifupa na mengineyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimechukua ombi lake Mheshimiwa Shangazi la kutaka watu wa kule Mlalo waweze kupata mabwawa ya samaki ili waweze kufuga samaki ili waweze kupata faida ya kupata protein na virutubisho vingine.
Namhakikishia ya kwamba tutampatia wataalam watakaoweza kushirikiana na halmashauri yake, watakaoweza kwenda kufanya mapinduzi haya ya ufugaji wa samaki na watapata na vifaranga pia tena si vifaranga tu, vifaranga bora.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza kabisa naishukuru Wizara kwa lengo lake la kutoa semina kwa Waheshimiwa Wabunge kwa uelewa wa masuala ya uvuvi, lakini kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Mwanza ambao wananufaika na uvuvi wa Ziwa Victoria ambao wengi wao ni wanawake na vijana, napenda kuuliza maswali yangu mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa changamoto nyingi za uvuvi zinatokana na sera na sheria zilizopitwa na wakati ikiwemo Sheria ya mwaka 1972 inayohusisha masuala ya nyavu; je, ni lini Serikali itakaa kuzipitia sheria hizi kwa lengo la kuzirekebisha? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; licha ya Ziwa Victoria kutumika na nchi tatu, yaani Tanzania, Kenya na Uganda, bado kila nchi imekuwa na sera zake juu ya uvuvi. Je, ni lini Serikali itaanzisha mchakato kuhakikisha kwamba kunakuwa na sera moja ya uvuvi katika Ziwa Victoria yaani One Lake, One Policy? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Maria Kangoye kwa kuweza kusimamia vyema kabisa maslahi mapana ya wananchi waliomtuma wa Mkoa wa Mwanza wakiwemo vijana na akina mama. Hongera sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameniuliza maswali mawili; la kwanza ni juu ya mapitio na maboresho ya Sheria ya Uvuvi. Naomba nimhakikishie kwamba sheria ile aliyoitaja ya mwaka 1970, Sheria Namba 6 ya Uvuvi tayari ilishaboreshwa, ndiyo maana tuna Sheria Namba 22 ya mwaka 2003 ambayo inakwenda na kanuni zake za mwaka 2009 ambayo na yenyewe sasa tuko katika hatua ya kuiboresha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa tunavyozungumza, wataalam wetu katika ngazi ya Serikali, IMTC kwa maana Makatibu Wakuu wanaijadili na baadaye itaingia katika vikao vyetu vya Baraza la Mawaziri ili kuweza kuboreshwa zaidi na hatimaye kwa maslahi mapana ya sekta hii ya uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtoe hofu Mheshimiwa Maria Kangoye kwamba Sheria yetu ya Uvuvi kabla ya mwaka huu wa 2018 haujakamilika, tutahakikisha kwamba inaingia humu Bungeni kwa ajili ya kuweza kupata baraka na kuboreshwa zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni juu ya sera moja ya uvuvi, kwa maana ya kwamba Ziwa Victoria ni ziwa ambalo liko shared na nchi tatu, kwa maana ya Tanzania, Kenya na Uganda ambapo sisi kama Tanzania ndio tunaomiliki eneo kubwa la Ziwa Victoria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli na nimwambie tu kwamba katika siku ya tarehe 2 Machi, 2018 Mawaziri wa nchi hizi tatu akiwepo Waziri wetu Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina alishiriki katika kikao ambacho kilikwenda na maazimio.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya maazimio makubwa kabisa ni kuhakikisha kwamba katika kila nchi, zile taasisi zetu za utafiti zinafanya utafiti na kuweza ku- compromise (kuweza kwenda kwa pamoja) juu ya sera zetu, sheria zetu ili zisiweze kugongana; ili wavuvi wote wanaoshiriki shughuli za uvuvi katika Ziwa Victoria wawe wanajua kwamba sheria hii hapa Tanzania, Kenya au Uganda ni sawasawa bila kuvunja sheria za nchi nyingine.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu haya yenye kuleta matumaini kwa wavuvi wetu, lakini yametuelekeza namna ambavyo Serikali inaendelea kulinda mazingira ya bahari na kuendelea kulinda viumbe vilivyopo ndani ya bahari na kuendelea kuleta tija kwa wavuvi wetu. Sasa napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo ya Lindi Manispaa, Lindi Vijijini maeneo ya Kilwa, vijana sasa wameamua kujitengenezea ajira kupitia shughuli za uvuvi na tayari wamejiunga katika vikundi mbalimbali. Napenda kujua ni lini sasa Serikali itakuja kuwawezesha angalau kuwapa fiber boat na injini za boti ili vijana wale waendelee kuwa na uvuvi wa tija na kuongeza vipato vyao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, napenda sasa Serikali ituambie italeta lini mwongozo ambao utatuelekeza ni nyavu zipi zitatumika katika maziwa, mito na bahari. Unaposema kutumia nyavu ya nchi mbili, samaki wa baharini ni tofauti na samaki hao wa maziwa. Kwa mfano baharini kuna chuchungi…
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna dagaa, lakini unaposema tutumie nyavu ya nchi mbili maana yake samaki wale huwezi kuwapata. Napenda Serikali iseme ni lini itatuletea mwongozo wa namna nyavu zitakavyotumika zile za bahari, maziwa pamoja na mito?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hayo ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza nampongeza sana kwa ufuatiliaji wake wa karibu wa masuala yanayohusua wananchi na hasa wavuvi wa kule Lindi. Anauliza lini Serikali itawawezesha vijana, nataka nimhakikishie tu kwamba Serikali iko tayari, tunapokea maombi hasa yanayohusu vifaa kwa maana ya injini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari wiki iliyopita tumeshapokea maombi kutoka kwa Mheshimiwa Mbunge wa Lindi anayeitwa Mheshimiwa Hamidu Bobali akiomba mashine kwa vikundi viwili. Kwa hivyo, nafahamu Mheshimiwa Hamida ni Mbunge makini na yeye namkaribisha ofisini kutuletea hayo maombi na mashine zipo kwa ajili ya kuweza kuwasaidia vijana na vikundi vya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni lini Serikali itaweka mwongozo wa matumizi ya nyavu katika maeneo mbalimbali. Tunafikiria mwaka huu kuleta maboresho ya sheria lakini kwa maelezo zaidi na kwa uelewa mpana zaidi wa sekta hii ya uvuvi Wizara yetu imeandaa semina kwa Wabunge wote ambayo itakwenda kujibu masuala yanayohusu tasnia nzima ya uvuvi siku ya Jumapili na tunawakaribisha Waheshimiwa Wabunge muweze kushiriki kikamilifu katika semina hii. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwa kuwa zoezi hili la kuzuia uvuvi haramu linatumiwa sasa na vikosi vya doria kunyanyasa, kudhalilisha na kupora wananchi hasa wavuvi kwenye Visiwa vya Ukerewe kwa kuwadai pesa na malipo mbalimbali yasiyo halali. Nataka kujua Serikali iko tayari kutoa kauli kuzuia unyanyasaji huo lakini na Mheshimiwa Waziri kufika Ukerewe kukaa na wavuvi na kupata ushahidi wa haya yaliyotokea ili Serikali iweze kuchukua hatua kwa wahusika? Nashukuru. (Makofi)
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa swali la Mheshimiwa Mbunge wa Ukerewe. Naomba kusema kwamba kama kuna changamoto yoyote ambapo watendaji wetu kwa namna ile wameenda kinyume na misingi na taratibu tulizowapa, watendaji wetu wote wanapoenda doria wanapewa mwongozo wa makosa gani ambayo yanatakiwa kuchukuliwa hatua na kwa kiasi gani. Mheshimiwa Mbunge kama anayo hiyo orodha ya watu ambao anasema kwamba hawakutendewa haki atuletee sisi tutalishughulikia mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mimi kwenda Ukerewe…
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo ya uvuvi haramu katika maeneo ya Lindi yanafanana sana na matatizo ya uvuvi haramu katika Kisiwa cha Mafia. Taasisi iliyopewa mamlaka ya kushughulika na uvuvi haramu Mafia imejitwika majukumu mengi zaidi ya uhifadhi kwa maana ya wanauza maeneo ya vivutio na kukusanya mapato. Je, ni lini sasa Serikali itahakikisha kwamba Taasisi ya Hifadhi ya Bahari ya Mafia wanabaki na kazi ya uhifadhi peke yake badala ya kujishughulisha na kukusanya mapato? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Hifadhi ya Bahari kwa Kiingereza tunaiita kwa kifupi MPRU ipo kwa mujibu wa sheria za nchi. Miongozo ya kuanzishwa kwake MPRU kwa maana ya hifadhi ya bahari inawaelekeza kufanya kazi kadha wa kadha.
Moja ya kazi hizo ni uhifadhi lakini mbili ni kusimamia masuala yanayohusu wanaokuja katika maeneo yale ya hifadhi ikiwa ni pamoja na kuwatoza ushuru ambao kwa pamoja unarudishwa katika vijiji na Halmashauri ya Wilaya ya Mafia kwa mfumo wa asilimia 30. Asilimia 10 inakwenda katika halmashauri ya wilaya na asilimia 20 inakwenda moja kwa moja katika vijiji vinavyohusika na uhifadhi ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la Mheshimiwa Mbunge ni lini sasa MPRU itajielekeza katika kusimamia uhifadhi tu badala ya kukusanya ushuru. Masuala haya ni ya kisheria na kikanuni tunamkaribisha Mheshimiwa Dau kwa hoja hiyo mahsusi kabisa ya kutaka kwamba MPRU ijielekeze na uhifadhi tu badala ya kufanya shughuli zingine ikiwemo hiyo ya kukusanya mapato. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri na jinsi ambavyo Serikali imejipanga kuwawezesha wavuvi. Vilevile wapo wavuvi ambao hawana uwezo kabisa, wanahitaji kuwezeshwa na Serikali. Ningependa kujua sasa nini mkakati wa Serikali wa kuwapatia ruzuku wavuvi hawa ili waweze kujikwamua kiuchumi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; wavuvi walioko katika Mkoa wa Geita hasa katika Jimbo la Busanda katika maeneo ya Bukondo, Nyakasamwa pamoja na Nungwe wanazo changamoto nyingi. Ningependa kujua Mheshimiwa Waziri ni lini atakuja kututembelea katika Jimbo la Busanda ili kubaini changamoto hizi na kuweza kuzitafutia ufumbuzi wa kutosha? Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza linahusu ruzuku kwa wavuvi. Wizara inayo program maalum ya kuwawezesha wavuvi ambao wapo katika utaratibu wa vikundi ambapo tunatoa mashine za ruzuku, wao wenyewe wavuvi wanachangia asilimia 60 na Wizara tunachangia asilimia 40.
Mheshimiwa Spika, hivyo, shime Mheshimiwa Mbunge aende akawahamasishe wavuvi wake waweze kuwa katika vikundi, wapitishie barua zao za maombi kwa Halmashauri ya Wilaya kwa maana ya Mkurugenzi na hatimaye azilete Wizarani, tunamhakikishia Mbunge kumsaidia kuweza kupata mashine hizo kwa ajili ya vikundi vyake.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Lolesia Bukwimba, bibi yangu huyu anaomba niende kuwatembelea babu zangu kule Busanda. Nataka nimhakikishie kwamba baada ya Bunge hili mimi na yeye mguu kwa mguu mpaka Busanda kuhakikisha nakwenda kukutana na wavuvi wa kule Busanda. Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. MARY D. MURO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa hekta 270 za shamba hilo kuongezwa haziwezi kukidhi mahitaji ya wananchi wa Mkoa wa Pwani pamoja na Mkoa wa Dar es Salaam wanaotumia majani hayo, je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza zaidi ya hapo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hei imekuwa bei aghali, je, Serikali ina mpango gani wa kupunguza bei ili kuvutia wananchi wengi kutumia majani hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza anataka kujua kwamba hizi ekari 270 ni ndogo kuweza kukidhi haja ya mahitaji ya chakula cha mifugo kwa Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Dar es Salaam, je, Serikali tumejipangaje? Jibu la swali hili ni kwamba Serikali tumejipanga vizuri na ndiyo maana tumehakikisha kwamba maeneo yetu ambayo ni ya mifugo likiwemo hili la Vikuge na mengineyo yale ya Holding Grounds na hata maeneo yetu ya NARCO pale Ruvu tunawekeza sana sasa hivi katika kuhakikisha kwamba tunapata maliso ya kutosha ili kuweza kuwa-supply wafugaji wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na swali la pili ni juu ya bei; ni kweli, bado bei za hei na mbegu za malisho ziko juu. Hivi sasa tupo katika hatua ya mwisho kama Serikali ya ku-certify mbegu za malisho ili nazo ziweze kuuzwa kama zinavyouzwa mbegu za mahindi, mpunga na mazao mengine ili kuwawezesha wafugaji wetu waweze kupata mbegu hizo kwa bei nafuu. Hivi sasa bei ya kilo moja ya mbegu za malisho ni takribani shilingi 17,000. Mkakati wetu ni kuhakikisha kwamba zinashuka ili ziweze kuwasaidia wafugaji walio wengi.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nimepokea majibu ya Naibu Waziri. Kwa kuwa ametoa ahadi na bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi inakuja tarehe 17 Mei,2018 na tarehe 18 Mei, 2018, nitajiridhisha kwenye vitabu vyao kama kweli wametenga na wameingiza kuhusu ujenzi wa malambo ndani ya Jimbo la Mlimba.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, nampongeza Mkurugenzi na Halmashauri ya Kilombelo angalau tumetenga sisi kwa mapato ya ndani shilingi milioni 103 kwa ajili ya kuboresha na kujenga malambo ndani ya Halmashauri na Jimbo la Mlimba. Hizo ni jitihada tunafanya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu linakuja, kwa kuwa, Jimbo la Mlimba lina takribani vijjiji 18 na kuna kilometa 606 eneo ambalo wafugaji wamekaa huko kwa wingi na vinaenda kufutwa, je, Wizara hii au Naibu Waziri yupo tayari sasa kwenda Jimbo la Mlimba kuangalia taharuki hii inayotokea kwa wafugaji hao na kuona umuhimu wa kuweka malambo ili wananchi hao na wafugaji wasiende kuingia kwenye haya maeneo ambayo yanachukuliwa na Serikali kwa ajili ya kupeleka maji kwenye Stiegler’s Gorge? Kuna taharuki kubwa sana ndani ya Jimbo la Mlimba. Je, yupo tayari sasa kwenda kuangalia na kupanga mipango sahihi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa ya kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Susan Kiwanga. Kwa ruhusa yako, naomba nimpongeze sana Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mlimba kwa kutenga pesa hizo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mifugo yetu inapata maji.
Mheshimiwa Spika, swali lake ni kutaka kujua kama niko tayari kwenda naye Mlimba kuangalia juu ya adha wanayopata wafugaji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi tunafahamu ufugaji ni maisha yetu na maisha yetu ni ufugaji. Hivyo, nipo tayari kwenda Mlimba kuungana naye kwa ajili ya kwenda kuwaona wafugaji hawa.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali madogo ya nyongeza. Kwanza nianze kumshukuru Waziri kwa majibu yake, lakini naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa huu mradi ni muhimu sana na una tija sana katika manispaa yetu na ni mradi ambao kwa kweli toka mwaka 2008 umeanzishwa na ni chanzo kizuri sana cha mapato kama ambavyo amesema kwenye jibu lake. Pia tulikuwa tunategemea kwamba kama ungekamilika, ungeweza kutoa ajira zaidi ya 200 katika Manispaa na katika Mkoa mzima wa Iringa. Katika majibu yake, Serikali bado haijatoa commitment ya mradi huu kwa sababu tulikuwa tunategemea kwamba kama mradi huu ungekamilika kwa wakati…
Je, hiyo pesa ambayo inahitajika katika mradi huu Serikali inaji-commit vipi maana ni mradi ambao tunategemea kwamba utaweza kusaidia hata miradi mingine katika manispaa yetu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naomba kwanza nimpongeze Balozi wa Comoro, Mheshimiwa Mabumba kwa sababu aliweza kuwaalika wafugaji wanaotoka Tanzania kwenda kuona fursa zilizoko katika nchi ya Comoro na kwa kweli tuliona kuna soko kubwa sana la nyama, ng’ombe na la mbuzi. Je, Serikali sasa inawasaidiaje wafugaji kuunganishwa na masoko hayo katika nchi hiyo ya Comoro au nchi nyingine ili iweze kuleta tija katika nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza amezungumzia juu ya commitment ya Serikali katika kuhakikisha kwamba mradi huu wa machinjio ya Manispaa ya Iringa unaweza kupata pesa na hatimaye unakuwa ni chanzo cha mapato cha Halmashauri na kuzalisha ajira. Nimpongeze sana Mheshimiwa Ritta Kabati kwa kazi kubwa anayoifanya kwa ajili ya watu wa Iringa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama yeye mwenyewe Mheshimiwa Ritta Kabati unafuatilia vizuri ataona kwamba hivi sasa Serikali imekuwa ikifanya miradi ya kielelezo ya kusaidia Halmashauri zetu ziweze kujizalishia kipato chao wao wenyewe. Nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa aliyokwishaianza kwa ajili ya Maispaa za Mkoa wa Dar es Salaam na kwingineko katika Taifa letu. Zimetolewa pesa nyingi kwa ajili ya miradi ya kielelezo ikiwemo ya machinjio kama machinjio ya Vingunguti imepata pesa nyingi ili iweze kufanya vizuri na kuwa na tija. Nina imani kwamba baada ya kumaliza Dar es Salaam vilevile Serikali inaweza ikafanya kazi ya kuelekea katika maeneo mengine ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ameuliza juu ya namna sisi Wizara ya Mifugo na Uvuvi tulivyojipanga katika kuhakikisha wafugaji wetu wanapata masoko. Kama Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine watakuwa wafuatiliaji wazuri wataona kazi kubwa tunayoifanya. Katika kuhakikisha tunatangaza mifugo yetu na tunapata soko nje sisi katika Wizara tuna Idara inayoitwa Idara ya Huduma za Mifugo na Masoko na tunayo Bodi ya Nyama ambayo kazi yake ni kutafuta masoko nje ya nchi na kuitangaza nyama yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, tunatoa ushauri na kuangalia ubora wa nyama yetu ili iweze kupata masoko nje. Kusema ukweli hivi sasa tumekuwa tukipata masoko makubwa sana. Katika mwaka wa 2004 tulikuwa tunauza tani zisizozidi tatu, mwaka wa 2016/2017 tumeuza zaidi ya tani 1,000 za nyama nje ya nchi kutoka Tanzania. Mkakati wetu ni kuhakikisha tusiingize nyama ndani ya Taifa letu, badala yake sisi tuwe na uwezo wa kutoa nyama nje ya nchi. Kwa hiyo, tunaomba Waheshimiwa Wabunge, watuunge mkono kuhakikisha jambo hili kama Wizara tunaendelea nalo na tunaweza kufanikisha ajenda yetu ya Tanzania ya Viwanda hasa ile inayohusu mazao yetu ya nyama na samaki.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Mji wa Kibiti ina mifugo mingi ya ng’ombe. Je, Serikali ina mpango gani wa kuijengea machinjio ya kisasa, malambo na majosho ili kuondoa migogoro baina ya wakulima na wafugaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba Halmashauri ya Kibiti ina mifugo mingi sasa, ni ukweli mifugo mingi imehamia katika Mkoa wetu wa Pwani, Wilaya za Mkuranga, Kibiti, Rufiji, Kisarawe zimepata mifugo mingi sana mara baada ya Serikali kukubaliana kuhamishia mifugo kutoka katika Bonde la Ihefu na kuhamia katika Mikoa ya Kusini na sisi tumepata neema hiyo. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Ungando, kwa namna ambavyo tumejipanga katika Wizara ya Mifugo, tunataka tuhakikishe mfugo hii iende kuwa ni fursa kubwa sana kwetu sisi watu wa Mkoa wa Pwani. Ndiyo maana katika mwaka huu wa fedha wa 2018/2019 ambao bajeti yake tunakwenda kuisoma hapa karibuni ataona haya aliyoyauliza ikiwemo ya malambo na majosho, yatakwenda pale katika maeneo yetu ya Wilaya za Mkuranga, Rufiji na Kibiti, ni kwa sababu ya wingi wa mifugo tuliyokuwa nayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa tuna mifugo mingi sana na mkakati pia ni kuhakikisha tunapata eneo la uchinjaji na ku-process nyama. Hii ni kwa sababu pia tuna advantage kubwa ya kuwa karibu na soko la hiyo nyama yenyewe maana nyama kuitoa Kibiti, Rufiji, Mkuranga ama Kisarawe ni rahisi zaidi kuipeleka Dar es Salaam kuliko eneo lingine katika nchi.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba na mimi nimuulize Mheshimiwa Naibu swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyeiti, kwa kuwa machinjio ya Mazizini ni machafu sana na mazingira yake yako tete na yanahatarisha hata maisha ya watumiaji na Halmashauri pia haipati mapato kutokana na machinjio hayo. Je, Serikali ina mikakati gani kuboresha machinjio haya ya Mazizini ili na Halmashauri nayo ipate kipato?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba naomba tu nijibu kwa ujumla kwa sababu sijafahamu kwamba hayo machinjio ya Mazizini anazungumzia Halmashauri gani, lakini naomba nimhakikishie kwamba Wizara yetu imeendelea kuhakikisha kwamba machinjio yote yawe safi. Ndiyo maana sasa hivi tuna operation maalum ya ukaguzi ya kuhakikisha tunaweka utaratibu mzuri wa tasnia nzima ya mifugo ya nyama kuanzia katika machinjio na hata huko katika minada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili tumekuwa tukilifanyia usimamizi wa karibu kabisa ili tuweze kupata ithibati ya nyama yetu kwa sababu biashara hii ya nyama haiishii kwetu sisi wenyewe, ni sheria za kimataifa zinazoongozwa na Shirika la Kimataifa la Mifugo (OIE). Kwa hiyo, tunasimamia vizuri na nataka nimhakikishie tutafika Mazizini na kuhakikisha ya kwamba machinjio yale yanakuwa ya viwango kwa maana ya usafi ili nyama yetu inayotoka pale iweze kuwa bora wa mlaji.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Longido katika harakati za kujiongezea mapato ya ndani ya kuinua kipato cha wananchi wake walijenga mnada wa mifugo katika Kata ya Kimokouwa inayopakana na Kata ya Namanga iliyoko mpakani mwa Kenya na Tanzania ili pia kuwatengenezea wachuuzi wa mifugo mazingira rafiki ya kuweza kufanya biashara ya mipakani (cross border trade) na kwa kuwa baada ya Halmashauri kumaliza mnada ule wakaanza kuhamasisha wananchi waliokuwa wanapitisha ng’ombe maporini kupeleka kuuza katika minada ya Kenya ambayo ndiyo inayutumika katika maeneo ya Longido, jana Waziri akaenda akatoa maagizo ya kuwapangia bei ya kulitumia soko lile kitendo ambacho kimewakera wananchi…
Naomba Waziri mwenye dhamana aliyekwenda jana kutoa directives za bei ya mifugo atoe kauli itakayowafanya wananchi wa Longido na Halmashauri kuelewa kwamba soko hili ambalo wamejenga kwa nguvu zao wenyewe na wafadhili bila Wizara kuwekeza hata shilingi watatoa justification gani ya kwenda kulitwaa na kulipangia bei ambayo sio rafiki ni kandamizi, hii ni sawa na kuvuna usichopanda?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tasnia hii ya mifugo inaendeshwa kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni zake. Tunafahamu kwamba Longido kumejengwa mnada kupitia miradi ya Serikali kupitia ule Mradi wa MIVAF unaosimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnada ule kimkakati uko mpakani na sisi katika tasnia hii ya mifugo kama Taifa kwa mwaka mmoja kwa tathmini tuliyoifanya ng’ombe 1,600,000 wanatoroshwa kwenda nje ya nchi. Pia tunapoteza jumla ya shilingi 263,000,000,000 kama Taifa ikiwa ni mapato yetu yanayotokana na tasnia hii ya mifugo hasa export royalty.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie Mheshimiwa Kiruswa kwa sababu nafahamu kwamba ni Mbunge makini na ana timu makini iliyoko kule ya DC na Mtendaji kwa maana ya Mkurugenzi, watupe ushirikiano. Hatufanyi jambo hili kwa ajili ya kuwakomoa, tunafanya jambo hili kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni za nchi yetu lakini tunafanya jambo hili kwa ajili ya kuhakikisha Taifa letu linanufaika na rasilimali zake. Ahsante sana.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Wananchi wa Mwaseni na Ngorongo walipewa ahadi ya ujenzi wa mabwawa katika maeneo hayo, je, ni lini Serikali sasa itajenga mabwawa hayo ili wananchi hawa wafaidike katika maeneo hayo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Kibiti imeshindwa kukusanya mapato yake ya ndani kutokana na matatizo yaliyotokea. Je, ni lini sasa Serikali itawajengea mabwawa wananchi hao ili waongeze kipato chao katika Halmashauri ya Kibiti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii ya kujibu maswali mawili ya nyongeza ya jirani na ndugu yangu Mheshimiwa Ally Seif Ungando na ninampongeza sana kwa jitihada kubwa anazozifanya za kuhakikisha kwamba maendeleo yanakwenda kule nyumbani kwetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza juu ya watu wa Mwaseni na Ngorongo kuahidiwa kupata mabwawa. Nataka nimwambie na niwaambie ndugu zangu wa Kibiti, Rufiji, Mkuranga, Kisarawe na Watanzania wote kwa ujumla, Kata za Mwaseni, Ngorongo na kata nyingine katika Wilaya ya Rufiji zitakwenda kuwa wanufaikaji wakubwa sana wa mradi mkubwa wa uzalishaji wa umeme wa Stiegler’s Gorge, mradi ambao utakuwa na matokeo chanya pia kwa sababu kutakuwa na eneo la ekari 140,000 kwa ajili ya kilimo. Vilevile katika bwawa lile tutakuwa na uwezo wa kuzalisha samaki wasiopungua tani 12,000 mpaka 20,000 kwa mwaka mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itakwenda kuwa na faida kubwa pia hata katika utalii kwa maana ya kwamba wapo watu watakaokuwa wanakuja kufanya kazi ya kuangalia bwawa lile kwa shughuli za utalii. Hivyo, niwaambie wananchi wa Kata hizi ya kwamba watakwenda kunufaika juu ya miradi hii ya mabwawa.
Kwa upande wa Kata za pale Kibiti pia kesho tunasoma bajeti yetu, namwomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira, asikilize mipango mikakati tuliyonayo katika suala zima la ufugaji wa samaki. (Makofi)
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na jitihada za Serikali za kuongeza zana za uvuvi katika sekta hii ya uvuvi na pamoja na kupongeza jitihada zinazoendelea. Ningependa kujua, pamoja na mwanzo huu mzuri uliofanywa na Serikali, je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuongeza wigo zaidi ili zana hizi zipatikane katika bahari yote ya Tanzania? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa sekta ya uvuvi ni miongoni mwa sekta ambazo zinaweza zikaleta tija katika Taifa letu na kuongeza Pato la Taifa, tumeshuhudia miaka iliyopita wakati Mheshimiwa Rais, Dkt. Joseph Magufuli, akiwa Waziri wa Uvuvi, alikamata meli moja tu na ikaleta tija kwa Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa kutengeneza meli za kutosha ili ziweze kwenda kuvua katika kina kirefu na kuongeza Pato la Taifa katika Taifa letu? (Makofi). Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana kwa kazi nzuri anayoifanya wakati wote ya kuwapambania wavuvi wa nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, anataka kujua juu ya mkakati wa Serikali wa kusambaza teknolojia hii. Katika jibu langu la msingi nimeeleza kwamba Taasisi yetu ya Utafiti ya TAFIRI inafanya utafiti wa kujiridhisha juu ya ufanisi wa teknolojia hii katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Mara tu baada ya kuwa tumefanikiwa na kujiridhisha kwamba teknolojia hii inaweza kutupatia tija, naomba nimhakikishie tutaisambaza kwa kiasi kikubwa katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu ikiwemo katika maeneo mengine ya bahari yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili, anataka kujua juu ya mkakati wa Serikali wa kupata meli kubwa kwa ajili ya kuweza kuvua na kupata faida kubwa kwa ajili ya nchi yetu. Naomba nimhakikishie kwamba Serikali tumejipanga vizuri na tupo katika programu ya kuhakikisha tunapata meli hiyo, hivi sasa tupo katika hatua kabla ya kwenda katika ununuzi wa meli hiyo, tuanzishe na kulifufua Shirika letu la TAFICO ambalo hili ndilo litakalokwenda kuwa msimamizi mkuu wa hata hiyo meli ambayo tunatarajia kuinunua.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba aendelee kuvuta subira na kutuunga mkono ilimradi tuweze kufikia katika hatua hii tunayoifikiria. (Makofi)
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ziwa Victoria lina samaki wa aina nyingi, ukiacha sangara tuna samaki aina ya gogogo, nembe na furu, lakini aina ya nyavu ambazo Wizara na Serikali inaruhusu kuvua ni nyavu ambazo zinavua sangara peke yake. Nataka Mheshimiwa Naibu Waziri aniambie hawa samaki wengine wanavuliwa kwa zana za aina gani, ikizingatiwa kwamba wanapatikana kwenye maji marefu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Ni kweli Ziwa Victoria lina aina nyingi ya samaki wakiwemo hawa aliowataja samaki aina ya gogogo, nembe na furu. Samaki hawa upo wakati ambapo hawakuwepo na ni kweli kanuni na sheria zetu haziwataji moja kwa moja samaki hawa. Hata hivyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tupo katika hatua sasa ya kuhakikisha kwamba samaki hawa nao wanatajwa na sheria na kanuni zetu ilimradi waweze kuingizwa katika hata vifaa vya kuweza kuwavulia na wananchi na wavuvi waweze kupata faida ya rasilimali hizi za nchi yetu. (Makofi)
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza madogo tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa adhabu hutolewa kwa wavuvi wanaovua kwa kutumia nyavu haramu. Je, kwa nini adhabu hiyo pia haiendi kwa yule anayemuuzia nyavu hizo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, ni lini Serikali itatoa elimu kwa wavuvi wetu ili na wao waweze kuvua kwa kuitumia bahari kuu ili iweze kuwanufaisha katika maisha yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii ya kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Fakharia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ametaka kujua kwa nini wale wanaowauzia na kuwasambazia wavuvi nyavu haramu hatuwachukulii hatua? Naomba nilihakikishie Bunge lako kwamba Wizara yetu imefanya kazi ya kuwachukulia hatua wote wanaouza na kusambaza na hata wanaozalisha nyavu hizo haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini juu ya suala la elimu, ni jambo endelevu, tumekuwa tukilifanya na tutaendelea kulifanya ili wavuvi wetu waweze kuendelea kunufaika na rasilimali zilizopo nchini.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nina maswali mawili mafupi.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa wavuvi wana-complain kuwa hawapati elimu ya uvuvi ambao unatakiwa na wanaopaswa kusimamia ni Afisa Ugani lakini mara kwa mara hawafanyi hivyo. Je, Serikali inafanyaje kusudi kuwapatia elimu ili hawa wavuvi waweze kuelewa ni nyavu zipi zinazotakiwa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa ufugaji wa samaki kwa kutumia mabwawa au fish ponds wananchi wameitikia kwa nguvu lakini bado hawajapatiwa elimu sawasawa. Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa elimu hii ya ufugaji wa samaki wa mabwawa ili kupunguza utapiamlo pamoja na kuinua kipato na kuhamasisha wananchi wa mikoa yote waweze kufuga ukiwepo na Mkoa wangu wa Morogoro maana hata wanawake wanaweza wakafuga kwa mabwawa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma na nichukue fursa hii kumpongeza sana kwa ufutiliaji na umakini wake katika kuona sekta hii ya uvuvi na kilimo zinasonga mbele.
Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza anataka kujua namna ambavyo sisi Serikali tumejipanga katika kuwasaidia wananchi wetu katika kupata elimu ya kujua ipi ni nyavu halali na ipi isiyokuwa nyavu halali, hasa ikizingatiwa kwamba Maafisa Ugani wetu hawafanyi kazi yao ipasavyo. Nataka nimhakikishe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imejipanga vyema na ndiyo maana katika mabadiliko na maboresho ya sheria ambayo tunakwenda nayo katika mwaka huu, katika jambo moja kubwa tutakalolifanya ni pamoja na kuhakikisha tunaziboresha BMUs zetu, kwa sababu BMUs ni mali ya wananchi wenyewe na zinachaguliwa na wananchi wenyewe. Tuna hakika kwamba kwa kufanya hivyo tutakuwa tumewafikia wananchi, wapeane elimu waweze kujua.
Mheshimiwa Spika, lazima niseme ukweli kwamba bahati nzuri nyavu zinazotumika ni chache. Kwa mfano, nyavu ya dagaa kwa upande wa ziwani inafahamika wazi kwamba ni nyavu inayotakiwa kuwa na jicho lisilozidi au lisilopungua milimita nane. Kwa hivyo, mtu anapokwenda akanunua nyavu inayoshuka chini ya ukubwa wa milimita nane hilo jambo tayari amevunja sheria. Kwa upande wa baharini, inafahamika wazi kwamba ni nyavu isiyopungua ukubwa wa milimita 10. Kwa hivyo, kwa wavuvi ambao hiyo ndiyo shughuli mara nyingi wamekuwa wakifahamu.
Mheshimiwa Spika, swali la pili anataka juu ya mkakati wetu kama Serikali. Naomba nimhakikishie habari njema kabisa kwamba sisi kama Serikali katika moja ya jambo kubwa tunalokwenda kulifanya sasa ni kuhakikisha vituo vyetu vyote vya uzalishaji wa vifaranga vya samaki nchi nzima, Kituo kama kile cha Morogoro pale Kingolwira na vingine vya Luhira kule Songea na Mwaipula kule Tabora vyote tunakwenda kuviboresha ili tuweze kuzalisha vifaranga vya kutosha na hatimaye wafugaji wetu waweze kuvipata.
Mheshimiwa Spika, lakini lingine ni kuhakikisha tunakwenda sambamba na wenzetu wa Wizara ya Fedha kwa sababu tumeshapeleka mapendekezo yetu ya kupunguza tozo na kodi mbalimbali ambazo ndizo zimekuwa kikwazo katika uwekezaji kwenye eneo hili la ufugaji wa samaki. Naomba tu Mheshimiwa Mbunge na wadau wengine wote waendelee kujipanga kuhakikisha kwamba huko iko fursa ya kuendeleza sekta hii ya uvuvi.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa Wabunge wenzangu watakubaliana na mimi kwamba hakuna mtu anayeunga mkono uvuvi haramu na sisi tunaotoka Kanda ya Ziwa tumekua kutokana na samaki. Kitu ambacho tunahoji ni namna gani hii operesheni watu wasiowatakia mema wananchi wetu wanavyoiendesha.
Mheshimiwa Spika, nilimwambia Waziri Jimboni kwa Mheshimiwa Kangi watu walienda kuvunja mafriji (fridges) ma-frizer (freezers) na kuwakamata wale watu na kuchukua pesa zao kinyume na utaratibu. Hivi navyoongea jimboni kwangu juzi Polisi wamewavamia akina mama na kuwapiga mabomu wakishirikiana na Mkuu wa Wilaya. Swali langu, hivi ni kweli operesheni yenu inalenga kunyanyasa watu na mnatoa tamko gani kwa watu ambao wanafanya vitu vya namna hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza natoa shukrani kubwa sana kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuwa Bunge zima limetuunga mkono juu ya suala linalohusu uvuvi haramu, kwa sababu uvuvi haramu ni uharibifu wa maliasili za nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, swali lake linahusu ni kwa nini watu wanaotekeleza jukumu hili la operesheni dhidi ya uvuvi haramu wananyanyasa wananchi. Kwa heshima kubwa na taadhima nataka niseme kwamba tunachokifanya tunakiita kwa kifupi Operesheni Uvuvi Haramu, lakini sisi tunakwenda mbele zaidi na kupambana na biashara haramu ya mazao yanayotokana na uvuvi.
Mheshimiwa Spika, kesi anayoisema Mheshimiwa Ester Bulaya ni maalum, kwamba kuna tatizo la wananchi katika jimbo lake au jimbo la Mheshimiwa Kangi Lugola wamenyanyaswa katika mafriji yao. Naomba nimhakikishie kwamba Serikali ipo kuanzia katika ngazi za Wilaya, sisi tuko tayari kupokea malalamiko yote yanayohusu specific cases na kuyashughulikia.
Mheshimiwa Spika, nataka nimwambie tumewatuma kufanya kazi ya kudhibiti uvuvi haramu na biashara haramu ya mazao ya uvuvi na siyo kuwanyanyasa watu. Kwa hivyo, kama ipo kesi maalumu inayohusu mtendaji wetu amenyanyasa mtu, sisi tuko tayari kupokea kesi hiyo, kuichukulia hatua na hata kumchukulia hatua Mtendaji yeyote atakayethibitika kwamba amefanya vitendo vya uvunjifu wa maadili kwa kuwaonea Watanzania.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru na mimi kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, napenda kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa nini tusitumie uzoefu ambao tuliupata katika mradi wa MACEP ambapo zoezi la kuzuia uvuvi haramu lilikuwa linaenda sambamba na kuwawezesha wavuvi wetu kwa vifaa na zana bora ili waondokane na uvuvi haramu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Ghasia, kwamba kwa nini tusitumie uzoefu tulioupata katika mradi wa MACEP. Mradi wa MACEP ulikuwa ni mradi maalum uliofadhiliwa na Benki ya Dunia. Mradi ule ulikuwa unahusianisha vipengele vingi ikiwemo kuwawezesha wavuvi wetu ikiwa ni pamoja na kujenga miundombinu ya uvuvi katika Ukanda wa Pwani.
Mheshimiwa Spika, tunao Mradi unaoitwa SWIOFish hivi sasa ambao pia upo kwenye Ukanda wa Pwani. Moja ya jambo ambalo unafanya ni pamoja na kuwawezesha wavuvi, kuwafanyia capacity building kwa maana ya uwezo wao wa pamoja wa kijamii, lakini vilevile na kujenga miundombinu. Kwa hivyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi huu upo katika hatua za kati na katika hatua zake za mwisho nina imani tutafika katika hii hatua ambayo yeye ameipendekeza hapa.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.
Mheshimiwa Spika, Wizara imekuwa ikidhibiti nyavu haramu kwa kuzichoma, lakini tunajua kwamba uchomaji wa nyavu hizi za plastic huleta madhara makubwa sana kwa afya za binadamu kwa sababu uchomaji wa plastic huachilia sumu kali sana aina ya dioxin ambayo inaweza ikaleta madhara makubwa sana kwenye ini, figo, moyo na magonjwa mengine kwa binaadamu. Kwa nini Serikali isitafute mikakati mingine mahsusi inayotunza mazingira katika kudhibiti hizi nyavu haramu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kujibu swali la nyongeza la Mwalimu wangu Mheshimiwa Dkt. Semesi Sware ambaye amenifundisha, pamoja na mengine Sheria za Uvuvi za Mwaka 2003, Na.22 pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika Sheria ya Uvuvi inaeleza wazi kwamba ukikamata nyavu haramu ni kuteketeza. Sasa katika uteketezaji ndiyo yeye anasema tutafute njia nyingine siyo ile ya kuchoma moto kwa sababu ukichoma moto ule moshi unakwenda kuathiri wanaadamu. Mimi nadhani tutalichukua jambo lake hili na tutalifanyia mkakati mzuri wa kuhakikisha wakati tunachoma basi ule moshi usiende kuathiri watu wengine wanaozunguka jamii ile. Ahsante.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Dhana ya uvuvi haramu imeenea sana kwenye kauli za Mawaziri, lakini kule ziwani kuna aina za samaki kama 30 na samaki pia wana makuzi tofauti, ni kama binadamu. Ukichukua umri wa Musukuma ukachukua na umri wa Mwalongo, tuko sawa, lakini ukituangalia kwa maumbile tulivyo tuko tofauti na unapotupa nyavu ziwani inakuja na samaki za aina tofauti wakiwepo wenye tabia kama yangu na Mwalongo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ukiwapima kwenye rula hawalingani lakini umri ni mmoja. Kwa kuwa sheria yenyewe ndiyo inajichanganya, ni lini Wizara itakuja na sheria ambayo itam-favour pia mvuvi anapokumbana na matatizo kama ya maumbile ya binadamu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Waziri wakati operesheni hii inapoendelea, kumekuwa na tabia ya kukamata nyavu saa nne na zinachomwa saa sita. Mfano mzuri ni kwenye Kisiwa cha Izumacheri kilichopo Jimbo la Geita Vijijini ambapo Maafisa Uvuvi walikamata nyavu ambazo siyo haramu lakini wakanyimwa rushwa, wakachoma nyavu dakika 15 zilizofuata na nyavu hizi ni halali. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufuatana na mimi kwenda kusikiliza SACCOS hiyo na kutoa adhabu kwa wale waliohusika na suala hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la lini Serikali itakuja na sheria mpya itakayowasaidia wavuvi waweze kufanya shughuli zao kwa uzuri zaidi, hasa ikizingatiwa hili analolisema la kwamba samaki wako wa aina tofauti na ile nyavu inapoingia inakwenda kuzoa hata wengine wasiohusika.
Mheshimiwa Spika, Serikali tupo katika hatua ya mwisho ya maboresho ya Sheria yetu ya Uvuvi na itakapokuwa tayari itaingia humu Bungeni ambapo Waheshimiwa Wabunge watashiriki kikamilifu katika kuhakikisha kwamba sheria ile tunaiboresha kwa pamoja kwa maslahi mapana ya Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameeleza juu ya suala linalohusu nyavu, ya kwamba nyavu hizi zinapokamatwa ghafla tu zinachomwa moto na akanitaka kama niko tayari niweze kufuatana naye kwa ajili ya kuweza kwenda kuwachukulia hatua wale watumishi wa Serikali ambao wanatenda kinyume.
Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Musukuma na Waheshimiwa Wabunge wote na hata wananchi wote wanaoshughulika katika shughuli hizi za uvuvi, Wizara yangu tuko tayari kabisa sisi kama viongozi kwa specific cases kama hii anayoizungumzia Mheshimiwa Musukuma, tutakwenda popote pale na endapo tutabaini watumishi wetu wametenda kinyume sisi kama Mawaziri tuko tayari kuwachukulia hatua kwa ajili ya mustakabali mpana zaidi wa wananchi na wavuvi wetu. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa kuwa baada ya operesheni nyavu zinazotumika sasa ni mbovu sana, hazina kiwango na wala hazistahili kutumika kwa uvuvi, zinawatia hasara sana watumiaji. Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kupata nyavu zinazostahili, zinazoweza kukabiliana na mazingira ya Maziwa Viktoria, Tanganyika na mengineyo ili wavuvi wetu mbali na kupata hasara za kuchomewa nyavu wasiendelee kupata hasara za kununua nyavu kila siku chache zinapokuwa zinapita? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, juu ya suala linalohusu ubora wa nyavu, ni kweli Wizara yangu imepokea malalamiko kutoka kwa wavuvi kutoka pande zote za nchi yetu hasa wavuvi wa Ziwa Viktoria na tumekwenda kujiridhisha. Tupo katika utaratibu wa kuendelea kufanya tathmini ya hali hii. Nataka nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba tunashirikiana vyema na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa ajili ya kuweza kupata viwango halisi vya ubora wa nyavu zetu zinazozalishwa nchini.
Mheshimiwa Spika, pale itakapobainika kwamba liko tatizo juu ya ubora huu, la kwanza tutawataka ama tunawataka wazalishaji wetu waongeze viwango vyao vya ubora, lakini ikibidi sisi kama Wizara tuko tayari kutafuta mpango mwingine wa kuweza kuwanusuru wananchi wetu ili waweze kuendelea na shughuli hii ya uvuvi bila ya tatizo lolote.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyiongeza.
Mheshimiwa Spika, ajira kubwa sana ipo kwenye sekta ya kilimo na uvuvi na Tanzania tumejaliwa kuwa na rasilimali hii ya ziwa pamoja na bahari lakini majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri naona amajielekeza kidogo kutokujibu swali la msingi la Mheshimiwa Massaburi, ambaye yeye alitaka kujua pamoja na mafunzo yanayoendelea au mazungumzo yanayoendelea na EU nini mkakati wa Serikali kuongeza udahili wa hao wanafunzi? Maana yake 1,100 ni namba ndogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mikoa ya Kanda ya Ziwa ikiwemo Wilaya ya Busega ni wadau wakubwa sana wa Ziwa Viktoria na zoezi la uvuvi haramu limeathiri sana vijana na hawana ajira. Nini mkakati wa Serikari wa kuwasaidia vijana hawa ambao sasa hawana ajira waweze kupata ajira? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Raphael Chegeni, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ni juu ya mkakati wa Serikali wa kuongeza udahili. Kama nilivyojibu katika swali letu la msingi tumehakikisha tunaimarisha vyuo vyetu vilivyo chini ya Wakala huu wa Uvuvi kwa maana ya FETA vile vya Gabimori na kule Mwanza, Mtwara na Kigoma. Kwa hivyo, kazi kubwa tuliyonayo katika mwaka huu wa fedha ni pamoja na kwenda na mpango wetu wa kushirikiana na wenzetu wa European Union ili mradi tuweze kuongeza uwezo wa kitaasisi ambao utapelekea kuendelea kuongeza idadi ya wanafunzi katika vyuo vyetu lakini kuwa na uwezo wa kitaaluma na kiteknolojia pia. Kwa hivyo, Mheshimiwa Mbunge ahakikishe tu kwamba wanafunzi au vijana waliopo katika Jimbo lake wawe tayari na wao kuweza kuingia katika vyuo hivi hasa kwa yeye palepale Mwanza Nyegezi ambapo watapata elimu hii na kule Rorya vilevile.
Mheshimiwa Spika, swali la pili ni mkakati gani tuliona kama Serikali, baada ya kuendesha Opesheni Uvuvi Haramu na vijana wengi kuwa wamekosa ajira tunawasaidiaje ili waweze kurudi katika ajira yao. Mkakati wetu Mkuu ambao umeelekezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, Ibara ya 25 mpaka ya 27 ni kuhakikisha kwamba tunawaunganisha vijana hawa katika vikundi vya ushirika na kazi hii tumeshaianza.
Mheshimiwa Spika, kwa bahati njema sana tunashirikiana vyema na Shirika letu la Umma la Hifadhi ya Jamii ya NSSF, tunao mpango unaoitwa Wavuvi Scheme. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Chegeni kwamba niko tayari kwenda kutoa elimu hii na wataalam wangu pale Busega ili vijana wa pale Busega wajiunge katika ushirika, kisha waweze kupata faida ya kuweza kupata mikopo na faida zingine zinazotokana na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, nimekuwa nikihamasisha sana wananchi wa Mkoa wa Njombe hususani akina mama kufuga ng’ombe wa maziwa. Je, ni Serikali itawasaidia kina mama hawa wa Mkoa wa Njombe katika suala la kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya kusindika maziwa ili kuweza kuinua uchumi wa nchi yetu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, Tanzania tumebarikiwa kuwa na ng’ombe wengi sana, je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuweza kuanzisha mashamba ya ng’ombe wa maziwa katika Wilaya mbalimbali ikiwemo Wilaya ya Chato - Mkoani Geita, Wilaya ya Busega - Mkoani Simiyu na Kilolo - Mkoani Iringa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Mgaya, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Neema Mgaya. Katika hili aliloliomba Serikali na kuiuliza nini mkakati wake juu ya kuanzisha viwanda vidogo vidogo, yeye amekuwa champion wa jambo hili. Katika mwaka huu tumemshuhudia akiwapa support akina mama wa Mkoa wa Njombe kwa kuwapa vyerehani ambavyo tunavitafsiri kuwa ni viwanda vidogo, kwa hivyo nampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pili, nataka nimhakikishie tu kwamba Serikalini hasa Mkoa wa Njombe umekuwa ukipata faida kubwa sana ya ushirika wa vyama vidogo vidogo ambavyo vinafanya kazi ya usindikaji wa maziwa. Pale Mufindi viko vyama vidogo vidogo vingi sana. Naomba pia uniruhusu niwapongeze Wabunge wa Mufindi karibu watatu, Mheshimiwa Mahmoud Mgimwa, Mheshimiwa Mendrad Kigola na Mheshimiwa Cosato Chumi wa Mufindi. Nimekuta pale kuna vyama vingi vya ushirika na hivyo nataka nimuombe Mheshimiwa Neema Mgaya na yeye aweze kushirikiana na Wabunge hawa wa Majimbo waweze kuvisaidia vyama vile vya ushirika viweze kusindika maziwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili ni jambo linalohusu ni lini Serikali itakwenda kuanzisha mashamba katika Wilaya mbalimbali. Bahati njema sana katika wilaya hizi alizozitaja tayari tuna shamba kubwa katika Kanda ya Ziwa la Mabuki, ambalo lina ng’ombe wazuri na bora kabisa. Naomba nitangaze kwa Waheshimiwa Wabunge wote shamba letu la Mabuki sasa lina ng’ombe wa kuuza, wanyama na wa maziwa wazuri ambao kwa kusema ukweli hata wateja sasa wamepungua sana. Tunawahamasisheni karibuni mnunue ng’ombe pale kwenye shamba letu. Ng’ombe wazuri wanaanzia Sh.1,500,000 mpaka Sh.1,800,000 kwa ajili ya nyama na maziwa.
Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mgaya kwamba kwa upande wa eneo hilo tunalo shamba zuri na kwa Kilolo kule tuna shamba zuri lile la Sao Hill. Hapa Kongwa kwa Mheshimiwa Spika pia tunayo Ranchi yetu ya Kongwa ambayo ina ng’ombe wazuri na Spika na wananchi wa pale Kongwa ni miongoni mwa watu ambao wanaweza kufaidika kwa ng’ombe wale wazuri kwa ajili ya ufugaji bora. (Makofi)
MHE. ZAYNAB M. VULU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa kilimo cha mwani kimekuwa hatarishi kutokana na mazingira kinapolimwa na kinalimwa na wanawake wanaoishi katika visiwa na ukanda wa bahari. Kutokana na mazingira hayo hatarishi, je, Serikali ina mpango gani kupitia benki, mashirika au taasisi zinazoendesha masuala ya bima ili kuweza kwenda kuwafikia wanawake hao na kuwapa elimu ya kuweza kuwapatia fedha za kutosha ili waweze kujikwamua katika vifaa na halikadhalika kuweza kujikinga na athari zozote zinazotokana na kilimo hicho kwa kuwa kinakuwa baharini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kilimo cha mwani mavuno yake ni mengi sana kutokana na zao lenyewe linavyofyonza maji mengi, je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha viwanda vidogo vidogo ili zao hilo liweze kuchakatwa na kuweza kusafirisha kwa wingi na kupata bei inayoweza kumkomboa mkulima wa mwani? Mheshimiwa Spika, nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya mama yangu, Mheshimiwa Zaynab Vulu, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoani kwetu Pwani, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ni uhatarishi wa kilimo chenyewe cha mwani ambacho kinalimwa kama ulivyosema Msheshimiwa Spika ni pamoja na Jimboni kwangu Mkuranga katika Kata ya Kisiju kwenye Kisiwa cha Koma.
Mheshimiwa Spika, kwa bahati njema sana Shirika letu la Bima la Taifa (NIC) limekuja na mpango la kuhakikisha kwamba linaanzisha Bima ya Kilimo. Kwa hivyo, kwa kutumia dirisha hili la Bima ya Kilimo kutoka NIC na kwa kutumia mpango wetu wa ushirika kwa vikundi vya wakulima, naomba mimi na Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum mama yangu Mheshimiwa Zaynab Matitu Vulu na Wabunge wengine wakulima wa mwani tuwahamasishe wakulima wetu wa mwani kule vijijini wajiunge katika ushirika na hatimaye tuwaunganishe na Shirika letu la Bima ili kuweza kupata nafuu hii endapo litatokea lolote la kutokea.
Mheshimiwa Spika, jambo la pili ameniuliza juu ya viwanda vidogovidogo. Ni kweli kwamba tunahitaji kutengeneza viwanda vidogovidogo. Changamoto kubwa inayoonekana hivi sasa pamoja naye kusema kwamba uzalishaji ni mkubwa lakini kwa soko la kimataifa bado tunayo changamoto kubwa ya uzalishaji mdogo lakini na ubora wenyewe wa lile zao letu. Ndiyo maana tumeweka mkakati wa kuhakikisha tunazalisha zaidi na pili tunazalisha kilicho bora.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa viwanda vidogovidogo tumekuwa tukivisaidia sana pale Bagamoyo maeneo ya Mlingotini ni eneo mojawapo ambalo Wizara yangu inasaidia vidogovidogo. Kipo kiwanda kidogo ambacho kinafanya uchakataji na ku-pack mazao yanayotokana na zao hili la mwani. Sisi Serikalini tupo tayari kuhakikisha kwamba tunaendelea kuhamasisha uwekezaji katika viwanda vidogovidogo na kuwapa support wakulima wetu.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi.
Mheshimiwa Spika, wakulima wa mwani sasa hivi wanapata shida kutokana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi kwa sababu ya ule mfumo wa ukulima unafanyika katika maji mafupi, mazao yale ya mwani mengi yamekuwa yakifa kwa sababu ya joto la maji na mchanga. Napenda kujua nini mkakati wa Serikali kuwawezesha wakulima hawa ambao wengi wao ni wanawake waweze kufanikiwa katika kilimo hiki ukiangalia sasa hivi wanapata tatizo la mabadiliko ya tabianchi uzalishaji wa mazao yao unashuka chini? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mwalimu wangu Mheshimiwa Dkt. Sware Semesi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kutokana na mabadiliko ya tabianchi kilimo cha mwani ambacho kilikuwa kikifanyika katika maji mafupi sasa kinawalazimisha wakulima wa mwani wasogee na waende katika maji marefu. Je, mkakati wetu ni nini kuwasaidia akina mama hawa ambao wana vifaa duni vya kuwapeleka katika haya maji marefu. Mojawapo ya mkakati ni kusisitiza na kupatikana kwa zile kamba, tunayo teknolojia ya kamba za kisasa za kufunga mwani ule ili uweze kuwa imara zaidi na upate ubora zaidi. Pili, ni kuwapa vyombo kwa maana ya boti ama mashine za kuwasaidia kuweza kufika walau kina kirefu kidogo. Kwa hivyo, huu ndiyo mkakati wetu na tayari Serikali tunazo mashine za kukopesha vikundi vya wavuvi, ikiwemo wakulima wa mwani. Kwa hivyo, Wabunge wote tunayo kazi ya kuvileta Wizarani vile vikundi vyetu ili tuweze kuwakopesha kile tulichonacho ili waweze kusogea katika hayo maji marefu zaidi. Ahsante.
MHE. SILYVESTRY F. KOKA: Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nia njema ya Serikali kurejesha baadhi ya maeneo ya shamba la mitamba la Kibaha kwa wananchi, kuna eneo dogo ambalo wananchi wanalikalia linaitwa maarufu Vingunguti. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari mimi na yeye kwenda kukutana na wananchi ili kuona muafaka kati yao na shamba hili la mitamba?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa machinjio ya kisasa yaliyokuwa yanajengwa pale kwenye Ranchi ya Ruvu ina zaidi ya miaka minne haijaendelea na ujenzi na huku mahitaji ya nyama bora ni makubwa kwa Pwani na Dar es Salaam. Je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza ujenzi wa machinjio haya hata kwa ubia kati ya wananchi na Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza anataka kujua kama niko tayari kwenda Kibaha na nataka kumhakikishia niko tayari kwenda Kibaha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, anataka kujua nini msimamo wa Serikali juu ya machinjio ya kisasa ya pale Ruvu. Ni kweli mradi huu umekawia, lakini kupitia mradi wa uendelezaji wa sekta ya kilimo, Serikali ya Korea imeonesha nia ya kutukopesha dola za Kimarekani takribani milioni 50 ambapo hivi sasa utaratibu Serikalini unaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na moja ya miradi ambayo itakwenda kunufaika na pesa hizi ni pamoja na machinjio ya kisasa ya Ruvu ambayo haitaishia kaktiak kuwa machinjio tu, tutakuwa na Leather Complex ambayo itakwenda kutengeneza na uchakataji wa ngozi. Pia vilevile tutakuwa tayari kutengeneza bidhaa mbalimbali za ngozi kupitia mradi huu wa machinjio ya pale Ruvu. Ahsante.
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, moja ya matishio ya samaki aina hii ni anapoingia katika mitego ya wavuvi huwa anajeruhiwa kwa sababu wao wanakuwa hawamli lakini anapata majeraha katika kumnasua kwenye zile nyavu. Matokeo yake kwa kuwa ngozi yake iko very delicate, akipata michubuko anakufa. Sasa kwa kuwa samaki huyu ni wa season anapatikana kuanzia miezi ya mwanzo ya Septemba mpaka Machi, je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kutengeneza quota system ambapo msimu wa potwe maeneo ya Kilindoni anapopatikana papigwe marufuku ya kuvua samaki wengine ili kumnusuru samaki huyu kwa sababu huenda akaondoka Mafia? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, utalii katika Kisiwa cha Mafia una gharama kubwa sana. Kila mtalii anayeingia eneo la hifadhi ya bahari analazimika kulipa dola 24 kwa siku moja. Kutokana na ughali huu, inalazimisha baadhi ya watalii kuanza kushindwa kuja Mafia. Je, Serikali sasa ina mpango gani kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupunguza kiwango hiki cha entrance fees za kuingia maeneo ya marine park ili kuweza kuvutia watalii wengi kuja Kisiwani Mafia? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya kaka yangu Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau kama ifuatavyo;
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri wa Utalii Mheshimiwa Hasunga kwa majibu mazuri ya msingi hasa pale aliposema anaitaka jamii iweze kushiriki kikamilifu katika ulinzi wa samaki hawa au papa huyu anayeitwa papa potwe ama pia ninachukua pongezi nyingi sana kwa kaka yangu Dau kwa kuwa mshirika mzuri wa kulinda rasilimali zetu za Taifa ambazo zimekuwa ni kivutio kikubwa cha watalii katika visiwa vyetu hivi vya Mafia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala alilolisema la kuweka utaratibu maalum Wizara yetu tunalichukua ili kusudi sasa tuwe na wakati wa uvuvi katika eneo la Kilindoni na kuna wakati ambapo tutazuia ili kuwapisha papa potwe waweze kustawi. Bila ya kufanya hivyo, papa potwe watahama Mafia na tutasababisha utalii wa papa potwe uweze kutoweka katika eneo hili la Mafia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili juu ya tozo mbalimbali ambzo zinachukuliwa na Wizara yetu kupitia kitengo chetu cha MPRU kwa maana ya hifadhi ya bahari na zile zinazokwenda Wizara ya Utalii, mimi naomba nimhakikishie kwamba sisi Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi na Wizara ya Maliasili na Utalii tutakaa kwa pamoja na kufanya review ya hizi tozo na kodi hizi zinazohusika katiak utalii huu ili kusudi tuweze kuhakikisha kwamba watalii waweze kuvutika kwa wengi zaidi. (Makofi)
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Ranchi ya Missenyi ni miongoni mwa ranchi za mifano na ina hekta 23,000 na ng’ombe 1,670. Je, Mheshimiwa Waziri anayo mambo mengine anayoweza kunieleza ili na mimi nianze kufikiria kama yeye kuiita Ranchi ya Missenyi ranchi ya mfano huku ikiwa na hekta 23,000 na ng’ombe 1,600? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa swali langu nimeuliza wananchi wanaozunguka Ranchi ya Missenyi wamepata faida zipi, sasa hii kusema mitamba 12 na mbuzi sita inanipa mashaka. Nimsaidie Mheshimiwa Waziri kwamba Kata ya Mabale ipo mbali, eneo tofauti kabisa na Ranchi ya Missenyi, Kata ya Mabale imezunguka Ranchi ya Mabale. Sasa yupo tayari kukubaliana na mimi kwamba waliomasidia kumtafutia majibu wamemdanganya na awawajibishe ili wasimdanganye tena? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimthibitishie kwamba ni kwa nini nimesema Ranchi ya Missenyi ni miongoni mwa ranchi za mfano katika nchi yetu. Nadhani yeye amechukulia kigezo cha idadi ya mifugo na ukubwa wa eneo pekee; lakini nataka nimwambie kwamba tuna sababu nyingine kadha wa kadha za kuifanya Ranchi ya Missenyi kuwa ni ranchi ya mfano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya sababu hizo ni eneo la kijiografia (geographical location) yake Ranchi ya Missenyi yenyewe. Sisi sote tunafahamu kwamba ranchi hii ipo katika mpaka wetu na nchi kadhaa zinazozunguka nchi yetu. Kwa hiyo, sisi kama Taifa na hata ambao waliasisi ranchi hii walikuwa wanajua kwa sababu gani ambapo tumeenda kuiweka ranchi hii. Hii ndiyo maana kutokana na sifa zake kadha wa kadha ambazo ni pamoja na hii ya idadi ya mifugo na geographical location tunasema kwamba Ranchi ya Missenyi ni ranchi ya mfano na tutaendelea kuiboresha ili kuhakikisha kwamba tasnia ya mifugo katika nchi yetu inaendelea kuwa na kipaumbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili amelieleza kuhusiana na Mabale kwamba haipo katika Ranchi ya Missenyi ama ipo mbali na Ranchi ya Missenyi na kwamba labda nimedanganywa na waandishi wangu wa majibu. Naomba nichukue maelezo haya ya Mheshimiwa Mbunge, na kama upo uboreshaji sisi tupo tayari kukosolewa maana kukosolewa ndiyo kuimarika pia, ahsante. (Makofi)
MHE. ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kama alivyosema Ranchi ya Missenyi ni ya mfano na huo mfano ni kutokuwa na mifugo.
Swali langu la msingi sababu inayosababisha Ranchi ya Missenyi isiwe na mifugo ni kwa sababu zile blocks mmewapa watu ambao siyo wafugaji wa mbali, wao kazi yao ni kukodisha. Je, kwa utaratibu mpya mlionao mtawajali wakazi wa eneo la Misenyi, kwamba ndio wapewe maeneo hayo ya ranchi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli kwamba palikuwa na kasoro kadha wa kadha ambazo zilisababishwa na kuwapatia watu ambao si wafugaji na matokeo yake wakawa wanakwenda kuwakodisha watu wengine. Hivi sasa baada ya kuingia sisi tumekubaliana kufanya mabadiliko na ndiyo maana tumezirudisha ranchi zile Wizarani kwa ajili ya kuanza kugawa upya na tumeanza kazi hiyo ya kupokea maombi, kuyapitia na kujiridhisha kwamba huyu kweli ni mfugaji na tuweze kumpatia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa faida tu ni kwamba pamoja na kufanya hivyo, tumekubaliana kwamba hatupo tayari kuona ng’ombe yoyote aliyepo katika maeneo yanayozunguka ranchi zetu anakufa kwa sababu ya kukosa malisho na maji, hivyo tumekubaliana ya kwamba wafugaji wanaozunguka pamoja na wafugaji wa Jimbo la Mheshimiwa Dkt. Diodorus Kamala waweze kulipia kwa muda wa miezi mitatu. Ng’ombe mmoja analipia shilingi 10,000 anaingia katika ranchi, anapewa eneo, ananenepeshwa na akimaliza anatoka badala ya ile kuendelea kuwapga faini kwa sababu ya kuingia katika eneo la ranchi. Hivyo, tumekubaliana kurasimisha hatua hizi.
MHE. HAMAD SALIM MAALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, pamoja na majibu ya Wizara bado nina maswala mawili ya nyongeza.
Pamoja na kuwa uvuvi si suala la Muungano, lakini uvuvi wa bahari kuu ni suala la Muungano, na kwa kuwa wavuvi wengi wa Visiwa vyetu vya Unguja na Pemba wanatumia uvuvi wa bahari kuu.
Je, ni lini Wizara ikishirikiana na Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu itatoa mafunzo kwa wavuvi wa Visiwa vya Unguja na Pemba ili waweze kuvua kwa ufanisi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili inaonesha kwamba uvuvi wa bahari kuu unakuwa unawasumbua sana wavuvi wetu wa Visiwa vya Unguja na Pemba ni juzi tu wavuvi zaidi ya 100 wamekamatwa nchini Kenya na sasa hivi wako ndani.
Je, ni lini Wizara ikishirikiana na mamlaka hiyo uvuvi wa bahari kuu itatoa vibali vya kudumu kwa wavuvi wetu wa Visiwa vya Unguja ili kuwaondolea usumbufu huo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza anataka kujua mafunzo na nataka nimhakikishie tu kwamba Taasisi yetu ya Usimamizi wa Bahari Kuu pamoja na Taasisi yetu ya Mafunzo ya Uvuvi (FETA) pale Mbegani Bagamoyo. Wanayo mafunzo wanayoyafanya kila mwaka, na hata mwaka jana kwa maana 2016/2017 wameweza kufundisha wavuvi takribani 150, kati ya hao 75 kutoka Visiwani na 75 kutoka Tanzania Bara. Kwa hiyo, hayo mafunzo huwa yanaendelea na hata mwaka huu 2018 yataendelea na mwakani 2019 yataendelea pia vilevile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni juu ya kadhia wanayoipata wavuvi wetu wa kutoka visiwani wanapokwenda kuvua maeneo ya jirani katika nchi ya jirani ya Kenya. Ukanda wetu sisi wa Tanzania ni mrefu sana tuna takribani kilometa 1424. Naomba niwasisitize sana wavuvi wetu wa Visiwa vya Unguja na Pemba watumie zaidi eneo letu ambalo Mungu ametujalia na lina samaki wengi zaidi. Lakini wanapotaka kwenda katika maeneo ya nchi nyingine sisi kama Wizara tuko tayari kushirikiana nao katika mamlaka zinazohusika ili kuhakikisha pia vilevile waweze kwenda kutumia fursa zinazopatikana katika maeneo mengine yanayotuzunguka.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nataka kuuliza swali la nyongeza.
Nimesikia katika majibu yake ametaja Mikoa ya Pwani, Tanga na Unguja, lakini Mtwara na Lindi ni miongoni mwa mikoa ambao wavuvi wapo na uvuvi unafanyika kwa wingi. Je, ni lini hiyo miradi ya majaribio itafika katika Mkoa wa Lindi na Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mama Hawa Ghasia ya kwamba baada ya kuonesha mafanikio katika maeneo tuliyoyataja mradi huu utatanuka hata kuelekea katika Mikoa ya Lindi na Mtwara ili wavuvi wa Lindi na Mtwara na wenyewe waweze kwenda kuvua na kupata mafaniko makubwa badala ya kutumia muda na rasilimali nyingi bila ya sababu.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ziwa Tanganyika ni ziwa ambalo lina kina kirefu na kufanya wavuvi wanaovua kwenye ziwa hilo kuwa na uvuvi wa kubahatisha. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wavuvi wa eneo la ziwa Tanganyika wavuvi wa Kasanga, Kirando, Karema, Ikola na Kalia na eneo zima la Mkoa wa Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niruhusu kwanza nimpongeze Mheshimiwa Moshi Kakoso kwa ufuatiliaji wake wa hali ya juu ya tasnia hii ya wavuvi na maendeleo ya wavuvi wa kule ziwa Tanganyika.
Kwa upande wa namna ambavyo Wizara tulivyojipanga kuwasaidia taasisi yetu ya TAFIRI imefanya utafiti ambao pamoja na kuwasaidia kuweza kufanya uvuvi wa tija. Lakini pia wavuvi wanakabiliwa na tatizo kubwa la upotevu wa rasilimali samaki kwa maana baada ya kuwavua post-harvest loss, tumewasaidia kwa kuwatengenezea majiko ambayo tunaita majiko bunifu. Haya majiko yanatumia jua na vilevile wakati wa masika wanatumia nishati kidogo sana ya kuni. Yameweza kuwasaidia sehemu kubwa ya Kigoma na tunakwenda katika mafanikio haya kuyapeleka vilevile katika sehemu za Mkoa wa Rukwa na Katavi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Moshi Kakoso ya kwamba tutawafikia.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda sasa Serikali imekuwa na mkakati wa kuchoma nyavu za wavuvi kwenye maziwa na kwenye bahari kuu wakisema nyavu hizo hazina viwango na kuwaongezea wavuvi wetu walio wengi umaskini. Tatizo hili ambalo Mheshimiwa Waziri mwenyewe alikuwa akijifahari kwamba tutaendelea kuchoma nyavu moto. Nini mbadala wa wavuvi hao kuwaondoa kwenye umasikini baada ya nyavu hizo kuzichoma moto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masoud kwamba nini mbadala wa kuchoma moto nyavu zile?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nyavu zile zimechomwa kwa mujibu wa Sheria Namba 22 ya mwaka 2003 na kanuni zake za mwaka 2009. Hatukufanya kwa ajili ya kumwonea mtu, ni kwa ajili ya ulinzi wa rasilimali zetu leo na hata vizazi vyetu vijavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mpango wa kuwasaidia; tunao mpango mzuri ambao unaitwa SWIOFish. Huu mpango utakwenda kujibu namna ya kuwasaidia wavuvi wetu wa ukanda wa Pwani kuweza kupata namna nzuri zaidi ya kuweza kutumia vyombo na zana bora zaidi za kuweza kufanya shughuli zao za uvuvi.
Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Masoud ya kwamba Serikali imejipanga. Hivi sasa mradi unafanyika na wao vilevile kule katika visiwa vya Unguja na Pemba utawafikia.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza na kabla sijauliza maswali yangu kwanza nipende kumpongeza Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kuinua sekta ya mifugo. Lakini hasa niishukuru Serikali kwa ajili ya soko hilo lililojengwa kule mpakani mwa Kenya na Tanzania katika Kijiji cha Eworendeke, na nitoe rai kwamba waachiwe halmashauri waendeshe kwa sababu ndio waliobuni Wizara itoe tu oversight.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza kwa kuwa jamii hii ya kifugaji ili mifugo iwaletee tija wanahitaji malisho, maji, tiba ya chanjo na kutibu magonjwa sambamba na masoko ya uhakika na ninashukuru kwamba soko la Eworendeke linaweza kuja kuwa soko la uhakika waondokane na adha ya kupeleka mifugo huko nje ya nchi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kutusaidia hasa wafugaji wa West Kilimanjaro waweze kupata hayo maeneo ya kulishia hasa ukizingatia kuna mgogoro mkubwa ambao umekuwa ukitokea kila wakati wa kiangazi kwenye yale mashamba pori yaliyotelekezwa na Serikali?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili linamhusu Waziri wa Maliasili kwa sababu maswali yangu yalichanganywa, kwa sababu niliuliza swali moja kwa ajili ya Wizara ya Utalii na majibu niliyopata sikuridhika nayo. Eneo lote la Wilaya ya Longido ni Pori Tengefu na dhana ya WMA ilipoanza mchakato ulifuatwa WMA ndiyo ikapatikana. Mchakato ukapitiwa…
Mheshimiwa Mwenyekiti, WMA ya Lake Natron imepitia mchakato wote. Ni kwa nini WMA hii haitangazwi na imebakia kutangazwa tu na kitu kinawezekana?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mbunge huyu mpya kwa kazi kubwa nzuri anayoifanya ya kuwasimamia wafugaji wa eneo hili la Longido.
Mheshimiwa Mwenyekiti, anataka kwanza, Mheshimiwa Mbunge namna ambayo tutakavyoweza kushirikiana nao kama Halmashauri, nataka nimhakikishie ya kwamba sisi kama Wizara tutawapa ushirikiano na hatutafanya kazi ile ya usimamizi wa moja kwa moja isipokuwa tutakuwa pale kwa pamoja kuhakikisha kwamba kodi zote za Serikali ambazo zinasimamiwa na Wizara zitakuwa zinapatikana kwa maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya suala la West Kilimanjaro, naomba nimhakikishie na niwahakikishie wafugaji wote wa eneo lile, ikiwa ni pamoja na Longido, Siha na kwingineko ya kwamba mkakati wetu mahususi wa Wizara ni kuhakikisha kwamba wafugaji ng’ombe hawafi tena. Wakati maeneo ya asili ambayo yanamilikiwa na Wizara yetu kwa maana ya ranchi ziko pale. Tumekubaliana ya kwamba wafugaji watapewa ruksa ya kupewa vitalu katika maeneo yale anaingiza ng’ombe wake, ng’ombe mmoja kwa kiasi cha shilingi 10,000; anamlisha, anamnywesha katika ranchi ile kwa muda wa miezi mitatu ananenepa na kumtoa kumpeleka sokoni.
Kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Kiruswa na wafugaji wote nchini ya kwamba tumejipanga vyema na tutawasaidia katika jambo hilo.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwa majibu mazuri aliyoyatoa.
Kuhusu hili suala la WMA kutangazwa katika lile eneo naomba kwanza niweke vizuri tu kwamba WMA ni hatua ya kwanza ya uhifadhi ambayo inashughulikiwa na vijiji vinavyozunguka maeneo ya hifadhi, baada ya hapo inakuja pori tengefu baada ya hapo pori la Akiba, baada ya hapo hifadhi ya Taifa. Sasa tumeshafika tayari kwenye pori tengefu hatuwezi kurudi tena chini kwenye WMA, lile eneo litaendelea bado kuwa ni pori tengefu, lakini baadae tutaangalia kama sifa zinaliruhusu kuwa ni pori la akiba baada ya hapo tutaendelea kupanda zaidi badala ya kurudi nyuma. (Makofi)
MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali kuhusiana na swali hili, hasa hasa ujenzi wa Kiwanda cha Maziwa kule Isange, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, wananchi wa Jimbo la Busokelo hasa Kata za Lupata, Kandete, Luteba, Mpombo, Isange, Lwanga, Kabula pamoja na Itete, wanafuga sana ng’ombe wa maziwa wapatao zaidi ya 35,000 na wanazalisha lita zaidi ya milioni 54 kwa mwaka lakini mbegu walizonazo bado ni ng’ombe wale wa zamani. Je, Serikali itawasaidiaje kupata ng’ombe wapya ambapo inaweza kufanyika kitu kinaitwa uhimilishaji kwa ajili ya uzalishaji zaidi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi hawa pamoja na ufugaji wao wanajitahidi sana kukusanya maziwa na kupeleka sehemu ambapo kuna matenki kwa njia ya baiskeli pamoja na pikipiki. Je, Serikali itawasaidiaje kutafuta ama kupata gari la kisasa lenye tenki ili liwasaidie kwa ajili ya kukusanya kwa wakulima na wafugaji ambao wanafuga ng’ombe hawa wa maziwa mpaka sehemu ya viwanda?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu swali hili, naomba kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mwakibete kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya ya kuhakikisha kwamba wapiga kura wake wa pale Busokelo Rungwe wanafanya kazi ya uzalishaji na kujenga nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameniuliza juu ya programu tuliyonayo kama Serikali ya kuhakikisha kwamba tunasaidia katika kuondoa kosaafu zile za kizamani na kuboresha kosaafu zetu mpya. Wizara yetu katika mpango mkakati wa mwaka 2018/2019, tumejipanga kuhakikisha tunazalisha ndama wa kosaafu hizi za kisasa wasiopungua milioni moja kwa kutumia njia ya uhimilishaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndama hawa milioni moja watakaozalishwa watatawanywa katika halmashauri zetu kwa ajili ya kuendeleza kosaafu mpya hizi zenye tija na thamani zaidi kwa uzalishaji wa maziwa na nyama. Moja katika halmashauri zitakazonufaika na mpango huu ni pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Busokelo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, ni namna gani tunaweza tukawasaidia wazalishaji wa maziwa kule Busokelo. Naomba nichukue fursa hii kuwapongeza sana wadau binafsi wanaoshirikiana vyema na Serikali na nampongeza pia Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri hiyo anayoifanya kuwashirikisha wadau hawa binafsi. Wadau wetu wa ASAS DAIRIES wanafanya kazi nzuri sana ya kuwaunganisha wazalishaji wa maziwa katika eneo hili la Busokelo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba wamepeleka vyombo vya usafiri kama pikipiki kwa ajili ya kukusanyia maziwa. Nafahamu pia ya kwamba wadau hawa wanayo malalamiko madogo madogo, sisi kama Wizara kwa kupitia Bodi yetu ya Maziwa tunafahamu malalamiko yao, tayari tunayafanyia kazi katika kuleta utengamanisho ili wazalishaji wetu waendelee kunufaika. Tunawashawishi sasa ASAS DIARIES badala ya kutumia pikipiki zile, waingize magari yenye cold storage waende kukusanyia maziwa ya wananchi wale ili wananchi waweze kupata faida zaidi ya uzalishaji wao wa maziwa haya.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mkoa wa Dodoma ni miongoni ya mikoa yenye mifugo mingi sana ikiwemo ng’ombe na kuna nyakati wafugaji wanakosa soko. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhamasisha wadau na wawekezaji mbalimbali ili waweze kujenga Kiwanda cha Maziwa na collection centre katika Mkoa wa Dodoma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wetu ni kuhakikisha kwanza vile viwanda vyetu tulivyonavyo vinafanya kazi ya kuchakata mazao ya mifugo. Hapa Dodoma tunacho kiwanda kikubwa cha TMC ambacho hivi karibuni utendaji wake wa kazi haukuwa mzuri sana lakini Wizara tumeingilia kati tunahakikisha kwamba kiwanda chetu hiki kinafanya kazi nzuri ya uchakataji wa mazao ya mifugo kwa maana ya uchinjaji na hatimaye kutengeneza zile nyama kwa ajili hata ya kuuza nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali lake ni kujua namna tunavyoweza kuwavutia wawekezaji wa Kiwanda cha Maziwa hapa Dodoma. Nataka tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wana Dodoma wote kwamba ombi hili la kuhakikisha tunakuwa na Kiwanda cha Maziwa hapa Dodoma tunalichukua na tutahakikisha kwamba Dodoma na yenyewe pia inakuwa centre nzuri ya kuhakikisha tunatengeneza mazao ya mifungo ikiwemo maziwa na kuyasambaza kote katika nchi yetu.
MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa nini operesheni za Serikali dhidi ya uvuvi haramu zimekuwa zikijikita katika kutekeza zana haramu za uvuvi badala ya kujikita katika kuwasaidia wavuvi hawa waweze kupata zana hizi halali kwa urahisi na kwa bei nafuu kwa kuwaondolea kodi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa uvuvi haramu unaelezwa kama moja ya tishio la kutoweka kwa samaki adimu kama ningu, nembe, gogogo, ngogwa, domodomo, sangara, njegele na sato katika Ziwa Victoria. Je, kuna mkakati wowote wa kusaidia samaki hawa kuzaliana tena ili kuendeleza fahari ya ziwa hilo na mazao yake?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini operesheni za Serikali zinajikita kuteketeza nyavu badala ya kuwapa nyavu halali? Operesheni za Serikali zinafanyika kwa mujibu wa sheria na operesheni hii inayofanyika kwa maana ya Operesheni Sangara inafanyika kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na.22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwapa nyavu za bei nafuu wavuvi ni utaratibu ambao tunao pia na ndiyo maana tumetoa punguzo la kodi na hata kuondoa baadhi ya kodi katika vifaa hivi vya uvuvi ili kusudi kuweza kuwasaidia wavuvi wetu. Kama haitoshi tumeanzisha programu maalum ambazo kwa kutumia hata Mifuko yetu ya kijamii kama vile NSSF kuwafanya wavuvi waweze kujiunga katika vikundi ili waweze kupata mikopo na kuweza kununua nyavu kwa bei nafuu na vifaa vingine kwa ajili ya shughuli za uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, ni kutoweka kwa samaki kama vile gogogo, nembe na furu. Tumeendelea kufanya tafiti mbalimbali kwa kutumia taasisi yetu ya utafiti ya TAFIRI ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kulinda rasilimali hizi za nchi kwa ajili ya vizazi vya leo na vizazi vijavyo. Tunawaomba Waheshimiwa Wabunge wote waweze kutuunga mkono katika jambo hili kwa manufaa mapana ya Taifa letu.
MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Serikali imekuwa ikichoma haya makokoro kila mara tani na tani, si muda muafaka sasa Serikali ikashughulika na wale wanaoingiza na wanaotengeneza hizi nyavu haramu nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inashughulika na ndiyo maana mwaka huu mwanzoni tumekamata nyavu nyingi sana za wazalishaji wa Sunflag kule Arusha ambazo tumeziteketeza. Tumeteketeza nyavu za waagizaji kutoka nje ya nchi badala ya ku-deal na wavuvi wadogo wadogo tu. Kwa hivyo, tunashughulika na wazalishaji, waagizaji na wauzaji pia.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Napenda kujua kwa nini Serikali haijikiti katika kuviimarisha Vikundi vya Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi yaani BMU’s ili kuweza kuwa na uhakika wa uendelevu wa usimamizi wa rasilimali hizi na wenye kuleta tija? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, BMUs zipo kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na.22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake lakini pia inatambulika na Sheria ya Ugatuaji wa Madaraka kwa maana ya D by D. Sisi tunaendelea kuzitumia BMUs na katika maboresho yetu ya sheria ambayo tunayategemea kuingia katika mwaka huu tutahakikisha kwamba tunazipa nguvu zaidi na mwongozo zaidi ili BMUs ziweze kufanya kazi vile ambavyo inatakiwa kwa sababu BMUs ni mali ya wananchi wenyewe.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Wilaya ya Kakonko ina wafugaji wa samaki waliojiunga kwenye vikundi katika Vijiji vya Nagwijima, Kasanda na Nyabibuye. Swali langu, Waziri yuko tayari kuwasaidia mikopo, ruzuku au chochote kile watu hawa ambao wametumia nguvu yao na nguvu ya Mbunge kutokana na Mfuko wa Jimbo ili waweze kuendeleza ufugaji wa samaki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tuko tayari kama Serikali kuwasaidia wafugaji wa samaki na ndiyo maana katika mapendekezo ya sheria na bajeti mwaka huu atakuja kuona kwamba tumependekeza kuhakikisha kodi na tozo mbalimbali zinazofanya tasnia hii ya ufugaji wa samaki isisonge mbele ziweze kupunguzwa ama kufutwa ili kusudi tuweze kuwasaidia wafugaji wa samaki.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
(a) Pamoja na majibu ya Serikali ambayo kwa kweli hayaridhishi sana na hayaendani hata na swali lilivyoulizwa, naomba tu sasa nipate kuuliza kulingana na majibu yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi milioni 4.8 alizotenga kwa ajili ya majosho katika vijiji vya Mkundi - Mtae na Kiwanja, haoni kwamba ni fedha chache sana kulinganisha na hizi shilingi milioni 12 zilizotengwa kwa ajili ya Vijiji vya Kamba na Kivingo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mtazamo huo, Serikali haioni kwamba haina dhamira ya kweli ya kuondoa kero kwa wafugaji?
(b) Kwa kuwa hakuna maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya maeneo ya malisho, hili nalizungumza mwezi wa Ramadhani nikiwa na uhakika; hizi beacon Serikali inazotaka kwenda kuweka, inaenda kuziweka katika maeneo gani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi kwa namna ambavyo anawapigania wananchi wake hasa kundi hili muhimu la wafugaji katika Jimbo lake. Swali lake la kwanza anataka kujua juu ya dhamira ya dhati ya Serikali katika kuwasaidia wafugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie kwamba Serikali inayo dhamira ya dhati ya kuwasaidia wafugaji na ndiyo maana katika bajeti yetu ya mwaka huu 2018/2019 ziko pesa tulizozitenga kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunatengeneza miundombinu ya mifugo na kwa upande wa swali la pili, anasema wapi tunakwenda kuweka hizo beacon?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango ya matumizi bora ya ardhi ipo katika Halmashauri na ardhi za vijiji zipo kwa mujibu wa Sheria Na. 5 ya Sheria ya Ardhi na Sheria Na. 6 ya Matumizi ya Ardhi. Kwa hiyo, namna ya kupanga na namna ya kutumia bado ipo katika mamlaka ya Serikali za Mitaa wao wenyewe ikiwa Mbunge yeye ni mmojawapo katika Madiwani ambao wanapaswa kwenda kusimamia na kushiriki katika upangaji wa matumizi bora ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie kwamba kwa upande kama Serikali Kuu tunayo sheria inayolinda maeneo hayo hasa ya malisho, Sheria Na. 13 ya mwaka 2010 inayohusu malisho ya mifugo. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie kwamba sisi kama Serikali tuna nia dhahiri na ya dhati kabisa ya kuwasaidia wafugaji.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa asilimia 95 ya wakazi wa Longido ni wafugaji na ndicho wanachokitegemea kwa uchumi wao; na kwa kuwa mvua kubwa za mwaka huu zimeharibu miundombinu ya mabwawa likiwemo bwawa la Kimokolwa lililopasuka, Emuriatata na Sinoniki; na kwa kuwa mabwawa mengine matatu yanayotegemewa…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri ana mpango gani au ametutengea fedha kiasi gani kurekebisha miundombinu hiyo iliyoharibika?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Kiruswa anataka kujua ni kiasi gani tumewatengea? Tunayo hela ambayo tumeitenga kwa ajili ya kuweza kuwasaidia wananchi wa Longido kwenda kurekebisha miundombinu yao ya mifugo ikiwa ni pamoja na mnada wa mifugo wa pale Longido.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la miundombinu iliyopasuka kutokana na mvua nyingi zilizonyesha nchini, naomba mimi na yeye Mheshimiwa Mbunge tuweze kukutana na kuweza kulijadili na kuona ni namna gani tutaweza tukatoka kwenda kuwasaidia wananchi.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kuuliza swali kwamba kwa kuwa tatizo kubwa la nchi yetu katika wafugaji ni suala la upatikanaji wa maeneo ya malisho na sheria ya mwaka 2010 ya Nyanda za Malisho Serikali ilishayaridhia.
Je, ni mkakati gani ya Serikali kuhakikisha kwamba kwa kutekeleza sheria hiyo inatenga maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na nashukuru kwa kunipongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria Na. 13 ya mwaka 2010 inatekeleza sheria mama za ardhi Sheria Na. 4 na Sheria Na. 5 ya mwaka 1999, lakini inatekeleza pia Sheria Na. 6 ya Matumizi ya Ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hizi zote zinataja kwamba umuhimu wa Serikali za vijiji kutambua wadau wanaokwenda kutumia ardhi zile na kuwatengea na kuwapimia na kuwamilikisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, bado inabaki kuwa ni kazi ya Halmashauri yenyewe, kisha kazi ya kutambua na kuwapa idhini ya kwamba hili ni eneo la malisho ni yetu sisi kwa kulingana na sheria yetu Na. 13 ya mwaka 2010.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wote….Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. PHILIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nami kwa kupata muda wa kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Ziwa Rukwa kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri huwa linafungwa kila wakati lakini pale Serikali inaporuhusu kufunguliwa bado samaki wale ni wadogo na wamedumaa kabisa na utafiti unafanywa lakini haufanywi ule utafiti wa wa kina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni zaidi ya miaka 20 sasa toka mwaka 1978 toka Serikali imepandikiza samaki Ziwa Rukwa. Nataka Mheshimiwa Waziri anijibu ni lini Serikali itafanya uthabiti wa kina kabisa wa uhakiki wa kuja kufanya utafiti katika Ziwa Rukwa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika skimu za umwagliaji nimeona hapa ameorodhesha maeneo ya Rukwa kule Sumbawanga, Mbozi pamoja na kule Momba lakini mimi nimeuliza Bonde la Songwe maana yake ni Jimboni Songwe, ni lini Serikali itakamilisha mradi wa Nanjembo ambao tayari usanifu ulishafanyika kwa ajili ya umwagiliaji, watupe fedha tuweze kufanya miradi ya umwagiliaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa ya kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, Mwalimu Mulugo na nashukuru pia kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua ni lini tutafanya utafiti wa kina, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, katika bajeti yetu ya mwaka huu, taasisi yetu ya utafiti ya TAFIRI tumeitengea pesa na tayari tumeshaielekeza kwamba katika moja ya kazi muhimu za kufanya ni kwenda kuangalia hatma ya Ziwa Rukwa na samaki wa Ziwa Rukwa ili waweze kuwanufaisha Watanzania wa kule Songwe. (Makofi)
MHE. KABWE R. Z. ZITTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini sasa Serikali itafanya utafiti iweze kutoa kanuni za kuwezesha uvuvi wa kisasa na viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi katika Mkoa wa Kigoma kuweza kufanyika? Lini utafiti huo utaweza kufanyika kwa sababu sio wajibu wa wananchi ni wajibu wa Serikali kufanya huo utafiti na miaka 21 imepita bila huo utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, sasa hivi kumekuwa na leseni nyingi sana za uvuvi. Mvuvi mmoja yaani kwa chombo kimoja kinahitaji leseni takribani tisa na hivyo kuongeza gharama kubwa sana kwa wavuvi wa Ziwa Tanganyika. Vilevile gharama za kuuza mazao ya uvuvi nje zimeongezeka kutoka senti 0.5 ya dola ya Marekani mpaka dola 1.5 kitu ambacho kinatufanya wavuvi wa Mkoa wa Kigoma kutokushindana vizuri na wenzetu wa Burundi na Congo kwa sababu wao hawana tozo hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni lini Serikali itahusianisha hizo tozo na kuzishusha ili tueweze kuendeleza export tunayoifanya sasa hivi ya mazao yetu kutoka Ziwa Tanganyika?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali linalouliza kuwa ni lini Serikali itafanya utafiti. Kupita taasisi yetu ya TAFIRI tumeanza hatua za awali za kufanya utafiti katika maji yetu ya Ziwa Victoria, lakini vile vile tunacho kituo cha TAFIRI pale Kigoma. Kwa hivyo hatua za mwanzo za utafiti huu kwa kushirikiana na nchi zinazozunguka Ziwa hili Tanganyika kupitia taasisi inayotuunganisha tutafanya utafiti pia wa kujiridhisha ya stock assessment na hatua za kuweza kuwaruhusu wawekezaji wakubwa, wakati na wadogo ziweze kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la ni juu ya leseni nyingi zilizopo. Uwepo wa leseni katika tasnia ya uvuvi
ni jambo la matakwa la kisheria lakini vilevile ya kitaalam. Kwa sababu inatusaidia hata kujua idadi ya wavuvi tulionao.

Naomba nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge juu ya tozo tunazozitoza kuonekana kuwa ni nyingi na kubwa na kutufanya tusiwe na ushindaji sahihi na wenzetu. Jambo hili ndani ya mamlaka yetu, tupo tayari kukaa na wadau kuweza kushaurina ili kuweza kufanya tasnia ya uvuvi iweze kuwa na manufaa kwa Taifa letu.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Ninampongeza na ninamshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jibu lake zuri ambalo limeleta uelewa na kuonesha nia ya kukufua ranchi zetu. Nilikuwa na maswali mawili ya ziada kama ifuatavyo:-

(i) Kwa kuwa katika maelezo yake amesema lengo kubwa ilikuwa ni kutoa mifugo bora kwa ajili ya nyama ndani ya nchi na kuuza nje ya nchi, na kwa kuwa Zanzibar inategemea kitoweo cha nyama kutoka Tanzania Bara, je,
Serikali ina mpango gani kupeleka nyama Zanzibar kwa utaratibu maalum?

(ii) Kwa kuwa Ranchi ya Ruvu likuwa inajengwa machinjio kubwa ya kisasa lakini mpaka sasa hvi imesimama na haijulikani itakamalika lini. Serikali ina kauli gani juu ya Ranchi hiyo ya Ruvu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya upelekaji wa kitoweo cha nyama ya ng’ombe Zanzibar hivi sasa wapo Watanzania wengi wanaofanya biashara ya kuchukua nyama ya ng’ombe na kupeleka Zanzibar na ziko kweli changamoto kadha wa kadha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mara changamoto tulizonazo huwa tunazifanyia kazi ya kuhakikisha tunazitatua na hatimaye kuweza kuwasaidia wenzetu kuweza kupata kitoweo cha nyama ng’ombe, mbuzi kwa uhakika na hilo tutaendelea kulifanya kadri litakavyokuwa likiibuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, juu ya machinjio ya Ruvu. Tupo kwenye mkakati mzuri wa kuhakikisha machinjio ya Ruvu inajengwa. Hivi sasa tumeshafanikisha kuona juu ya athari ya mazingira na hatua zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati tulionao ni kutafuta pesa ya kuhakikisha kuwa mradi ule unakamilika na kuwaweza kuwasidia Watanzania kupata nyama ya uhakika, lakini vilevile kuweza ku-export nje ya nchi na hata kutengeneza vitu vingine kama vile mazao yanayotokana na ngozi za ng’ombe wetu.
MHE. VEDASTUS M. MANYINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ningependa kuuliza maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili wale vijana wanaoishi kando kando wa ziwa waweze kuona umuhimu wa kutunza ziwa lao na kuzuia uvuvi haramu. Ni lini sasa Serikali itaweza kutenga fedha kwa ajili ya kuwasaidia kujenga mabwawa kando kando ya ziwa pamoja na cage ziwani ili ziweze kuwasaidi hao vijana katika kujipatia kipato ili waweze kuona umuhimu wa kutunza ziwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kila moja amekuwa akishuhudia akina mama wengi wanao nunua samaki wakiwa wamenyanganywa kwenye madishi yao, hata wale waliokaanga samaki wao wanaouza sokoni ambayo hii kusema kweli wao si wavuvi, lakini wanakuja kunyang’anywa samaki wale ambao wameshawanunua. Waziri anatoa kauli gani kuhusiana na unyanyasaji huu ambao unandelea katika baadhi ya maeneo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, mkakati wa Serikali tulionao wa kuhakikisha tunapunguza nguvu ya uvuvi katika maziwa na kuepusha vijana na uvuvi haramu katika kuhamasisha kufanya ufugaji wa samaki; tunaomkakati sana. Hivi sasa ninavyozungumza, tumeshaanza mkakati huo katika Ziwa Victoria ambapo wako watu binafsi walioanza ufugaji wa samaki katika vizimba lakini vilevile na sisi kama Serikali tumejiandaa kuhakikisha tunatengeneza incubators, kwa maana ya vikundi vya vijana ambavyo vitakwenda kufanya shughuli ya utengenezaji wa mabwawa lakini vilevile utengenezaji wa cages kwa ajili ya ufugaji wa samaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Manyinyi ahakikishe anawaunganisha vijana wake kama nilivyotangulia kujibu katika swali la awali, wakae katika vikundi vya ushirika, nasi Wizara ya Mifugo na Uvuvi tuko tayari kwenda kutoa elimu, lakini vilevile utaalam na kuhakikisha tunawasaidia vijana hawa kuwaongoza katika kufikia lengo sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni juu ya kauli gani tunatoa kwa ajili ya wale akina mama na wanawake wanaouza samaki katika mabeseni. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa tunalinda rasilimali za uvuvi. Katika lengo hilo, hatuko tayari kuona mwanamama anayefanya biashara ya uuzaji wa samaki katika mabeseni huko masokoni, anaonewa. Kama yuko Afisa wa Serikali anayekwenda kumsumbua na kumnyanyasa mwanamke anayeuza mafungu yake matatu, manne sokoni ya samaki, hii leo natoa kauli hapa katika Bunge hili Tukufu, jambo hilo ni marufuku. Kwa sababu lengo letu siyo kuangalia hawa samaki wanaowekwa katika mabeseni, lengo letu ni kutazama hasa kiini cha makosa haya yanayotokana na uvunjaji wa Sheria ya Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niwahakikishie tu akinamama wanaouza samaki nchini kote, wawe huru katika uuzaji wa samaki wao, wahakikishe kuwa wanapata kipato cha familia zao na kujenga Taifa letu.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Ng’ombe ni muhimu sana katika ustawi wa Taifa letu la Tanzania na hulipatia Taifa takribani 7% kutokana na ng’ombe hao. Kwa kuwa makundi makubwa yanaingia ndani ya Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Lindi; na kwa kuwa ng’ombe wanapoingia ndani ya mikoa hiyo huleta uharibifu mkubwa sana wa mazingira; na tunafahamu mazingira ndiyo kila kitu katika uhai wa binadamu; natahadharisha hii ili yasije yakatokea kama yale yaliyotokea kule Ihefu hatimaye yakasababisha mabwawa kukauka na maji yakakosekana ndani ya nchi yetu. Je, nini kauli ya Serikali au mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba mazingira yanaboreshwa ili yasije yakaleta athari kwa Watanzania na nchi kwa ujumla?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa mama Salma Kikwete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza mama yangu Mheshimiwa Salma Kikwete kwa kukiri na kukubali kuwa ng’ombe ni fursa kubwa sana kwa uchumi na ustawi wa Taifa letu. Kwa mtazamo huu wa kwamba ng’ombe ni fursa kubwa ya uchumi kwa Taifa letu, hivyo basi, ng’ombe ni fursa kubwa ya ustawi katika mikoa aliyoitaja ya Pwani na Lindi pia vilevile kwa uhamiaji wa ng’ombe wengi wanaoingia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tahadhari yake juu ya ulinzi wa mazingira, sisi Wizara ya Mifugo, tumeizingatia sana. Ndiyo maana mkakati wetu wa kuhakikisha kuwa tunalinda maeneo yanayotengwa mahususi kwa ajili ya wafugaji na kutoyasababishia kuhamishiwa kwa shughuli nyingine zozote za kibinadamu ikiwemo shughuli za kilimo, tutaendelea nao ili kuhakikisha tunalinda mazingira ya nchi yetu yasiharibiwe na vilevile kwa ustawi wa shughuli hizi za mifugo na shughuli nyingine za wananchi wetu.
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, je, Serikali ina mpango gani wa kujenga machinjio ya kisasa ili kuwaletea tija wananchi wa kibiti ambao sasa hivi wana mifugo mingi katika maeneo ya Makima, Nyatanga, Mwambao, Nyambunda, Msala na Muyuyu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, je, Wizara sasa haioni ina kila sababu ya kukaa na wakulima na wafugaji ili kubaini changamoto zao kutatua kama ilivyofanya katika Wizara ya Madini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Ungando, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, Mheshimiwa Ally Seif Ungando anataka kujua mkakati wa Serikali juu ya ujenzi wa machinjio ya kisasa kulingana na idadi ya mifugo iliyopo katika ukanda huu wa Wilaya ya Kibiti na jirani zake Mkuranga, Rufiji mpaka Kilwa. Jambo hili ni jema na Serikali imekuwa na mkakati huu ambapo baadhi ya maeneo katika Halmashauri mbalimbali nchini zimejengewa machinjio ya kisasa. Hivyo basi, ni wakati muafaka kwa Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti kuibua mradi huu wa kimkakati na nina hakika Serikali itakuwa pamoja kulingana na ukweli kwamba maeneo haya niliyoyataja hivi sasa yana fursa hii kubwa na nzuri ya Uhamiaji wa mifugo kwa wingi ambapo itakwenda kusababisha upatikanaji wa uhakika wa ajira vilevile kuongeza kipato cha Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili Mheshimiwa Ungando amenihimiza na kututaka Wizara yetu kukaa na wadau hasa wa ufugaji na wakulima, sawa na walivyofanya wenzetu wa Wizara ya Madini. Ni wazo jema na ni zuri sana. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Ungando na Waheshimiwa Wabunge wote, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa na utaratibu huo. Mara nyingi tumekuwa tukikutana na wadau wetu na hata sasa ninavyozungumza wako wataalam wetu kwa maana ya timu maalum inayoshughulika na migogoro ya wakulima na wafugaji, timu ambayo imeundwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi inayojumuisha wataalam kutoka Wizara ya TAMISEMI, Wizara ya Ardhi na Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi inayokwenda kusikiliza wakulima, kuwasikiliza wafugaji vijijini kwa ajili ya kuweza kupata suluhu ya migogoro yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi leo ninavyozungumza, timu ile ya wataalam iko katika Wilaya ya Kibiti ikifanya mazungumzo na wafugaji na wakulima kwa ajili ya kutafuta suluhu ya kudumu ya matatizo ya migogoro ya wakulima na wafugaji.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri kutoka kwa Naibu Waziri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imekiri kwamba itatoa mafunzo kwa wafugaji na Maafisa Ugani katika Halmashauri zetu, je, ni lini itatoa mafunzo hayo katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ambayo wafugaji wanaongezeka kwa kasi kubwa sana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru imetenga maeneo kwa maana ya vitalu vya wafugaji mbalimbali vinavyofikia 100; na kwa kuwa wakulima wengi wameshapewa maeneo hayo lakini mpaka sasa hawajaenda. Nini kauli ya Serikali kuhusu hawa wafugaji ambao wameshindwa kwenda kwenye maeneo yale ya wafugaji na kuendeleza migogoro na wakulima mbalimbali kwa mifugo yao kula mazao ya wakulima? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mpakate, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ni lini tutakwenda kupeleka mafunzo haya Wilayani Tunduru? Naomba nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba timu yetu iliyoko Kaliua ikitoka huko itakwenda Tunduru na Halmashauri zingine katika nchi yetu kwa ajili ya kutoa elimu hii kwa wafugaji na Maafisa Ugani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili analotaka kujua ni namna gani na tunatoa kauli gani kwa wale waliopata vitalu. Kwanza nataka niwapongeze sana viongozi wote wa kule Wilayani Tunduru kwa kazi kubwa waliyoifanya ya mfano ya kuandaa vitalu wao wenyewe Halmashauri na kuvigawa kwa wafugaji kwa ajili ya kufanya kazi ya ufugaji iliyo na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kauli ya Serikali ni kama ifuatvyo: Wafugaji wote waliopewa vitalu hivi na wakaacha kuvitumia kwa wakati, tunawapa tahadhari kwamba watanyang’anywa na watapewa wafugaji wengine walio tayari kufanya kazi hii kwa ufanisi.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awamu ya Kwanza Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Baba wa Taifa alisambaza mitamba bora katika maeneo yote ambayo yanafanya zero grazing. Kwa kuwa ni muda mrefu sasa na cross breeding imeshafifisha mazao yale ni lini sasa Serikali itaweza kuboresha na kutawanya mitamba bora, vifaranga bora vya kienyeji na vifaranga bora vya samaki katika maeneo ya wafugaji kama Kilimanjaro ambapo kuna wanawake wengi sana ambao ni wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shally Raymond, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza swali ni zuri sana juu ya Serikali kuhakikisha kwamba tunasambaza mitamba bora kwa wafugaji hasa akina mama wa Mkoa wa Kilimanjaro na Taifa zima. Progamu hii Serikali tunayo kupitia mashamba yetu ya mifugo yaliyosamba nchi nzima tunafanya kazi hii. Kwa mfano tu ni kwamba hivi karibuni kupitia dirisha letu la sekta binafsi tumewawezesha Ushirika wa Wafugaji wa Ng’ombe wa Maziwa Mkoani Tanga yaani TBCU, wamekopeshwa pesa na Benki yetu ya Kilimo ili waweze kununua mitamba bora 300 ambapo kufikia tarehe 30 ya mwezi huu mitamba ile itaenda kusambazwa kwa wafugaji wote wa Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, tuko tayari kuhakikisha kwamba na wafugaji wengine kote nchini wanapata fursa hii. Shime wafugaji wote wa ng’ombe wa maziwa, kuku hata wale wa samaki wajiunge katika vikundi ili waweze kutumia fursa hii inayopatikana kupitia dirisha letu la ukopeshaji la Benki ya Kilimo.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Nitumie fursa hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake na nimshukuru kwa ushirikiano ambao amekuwa anautoa kwa masuala ya uvuvi. Nina maswali mawili ya nyongeza; la kwanza uvuvi wa dagaa wanavuliwa kwa kuchotwa, kwa hiyo isitegemee kwamba wategemee dagaa wale wanase kwenye nyavu, ndio maana ni muhimu angalau matundu yake yawe madogo kidogo. Sasa kwa kuwa dagaa wanaopatikana Ziwa Victoria hawatofautiana sana na dagaa wanaopatikana Bahari ya Hindi na natambua kuna mchakato wa kufanya utafiti kwenye Bahari ya Hindi ili dagaa wanaovuliwa kwenye Bahari ya Hindi wavuliwe kwa nyavu za milimita sita na kuendelea. Je, Serikali haioni sababu sambamba na utafiti utakaofanyika Bahari ya Hindi ufanyike vilevile na uvuvi utakaofanyika Ziwa victoria kwa dagaa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wavuvi wa Ukerewe wa samaki aina ya gogogo au ngere wanapata bugudha sana wakati wanavua samaki wale kwa kisingizio kwamba sheria hairuhusu, lakini mazingira ya uvuvi wa samaki wale na aina yake ni tofauti sana na samaki wengine. Je, Serikali iko tayari sasa kutoa tamko ili wavuvi wa ngere kwenye Visiwa vya Ukerewe na maeneo mengine wasibughudhiwe ili wafanye shughuli zao za uvuvi wa samaki hawa bila shida yoyote. Nashukuru sana?
NAIBU WAZIRI MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Mkundi na timu ya Waheshimiwa Wabunge katika eneo la Ziwa Victoria kwa namna ambavyo mara kadhaa wamekuwa wakisimamia maslahi mapana ya wapigakura wa eneo hili ikiwa ni pamoja na kulinda rasilimali za nchi yetu kupitia sekta hii ya uvuvi. Sasa swali la kwanza la Mheshimiwa Mkundi linahusu juu ya ya Serikali kuwa tayari kufanya utafiti katika eneo la Ziwa Victoria kama ambavyo tunafanya utafiti kwenye maji ya bahari ili kuweza kuruhusu nyavu ya chini ya milimita nane kuweza kutumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kuwa, kwa upande wa bahari bahari zilizokuwa zikitumika ni milimita 10 na zimekubalika kuonekana na maoni ya wadau kuwa milimita 10 zimeshindwa kukamata dagaa na ndio maana Serikali tukaielekeza Taasisi yetu ya Utafiti (TAFIRI) kufanya utafiti na kujiridhisha ya kwamba tufanye mabadiliko ya kanuni kwa haraka ili ikiwezekana tuweze kutumia nyavu za milimita nane ili kuweza kuwabnufaisha wavuvi wa upande wa bahari.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa rai hii ya kutaka tutumie njia hiyo ya utafiti kwa upande wa Ziwa Victoria, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mkundi na Waheshimiwa Wabunge wote wavuvi wa kutoka Ziwa Victoria tunaichukua rai hiyo na tutawaelekeza TAFIRI waweze kufanya utafiti na kuweza kujiridhisha bila ya kuathiri sekta hii ya uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la Mheshimiwa Mkundi linahusu uvuvi wa samaki aina ya gogogo, ngere na ningu. Samaki hawa ni samaki wenye kupendwa sana katika eneo la Ziwa Victoria naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge katika mabadiliko ya kanuni tunayoyafanya hivi sasa tumezingatia kwamba tufanye makubaliano ya kuweza kupitisha kanuni rasmi sasa ya kuweza kuvua na kutumia rasilimali hii ya samaki hawa aina ya gogogo, ningu na ngere ambao wameonekana katika kanuni zilizopita kuwa hawakutajwa moja kwa moja. Naomba niwahakikishie wavuvi wote wa eneo la Ziwa Victoria Serikali inalifanyia kazi jambo hili na muda si mrefu watapata matokeo ili waweze ku-enjoy na kufurahia rasilimali za Taifa lao.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa kuwa katika Jimbo la Ngara hakuna maeneo yaliyotengwa kwa maana hakuna blocks kwa ajili ya malisho ya mifugo, sasa Serikali kupitia Wakala wake wa Mafunzo ya Mifugo Nchini LITA, wako tayari kuanzisha kituo hiki cha Incubation Youth Center katika Wilaya ya Ngara ambako kuna mifugo mingi zaidi ya Ng’ombe 75,000 ili kuweza sasa kuwawezesha vijana kuanzisha mashamba darasa ili waweze kujikimu kiuchumi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa upo mnada ambao Serikali iliweka fedha nyingi, mradi wa Mursagamba uliojengwa zaidi ya miaka 20 iliyopita, natambua kwamba Serikali imepeleka fedha sasa kwa ajili ya kukarabati ili uweze kuanza kutoa huduma, ni lini sasa mnada huu utafunguliwa ili uanze kutoa huduma?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Alex Gashaza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iko tayari kuhakikisha kwamba Chuo chetu cha LITA kilichopo pale Mkoani Kagera, katika Wilaya ya Karagwe katika ranch yetu kubwa ya Kikurura complex tutakitumia kwenda kufanya mafunzo ya hii program maalum ya Incubation Youth Center kwa ajili ya kuwanufaisha watu wa Wilaya ya Ngara, vijana mahususi kwa ajili ya kuweza kutumia fursa ya mifugo iliyokuwa mingi kuzalisha na kupata ajira na kuinua kipato chao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni juu ya mnada wa Mursagamba; ni kweli katika bajeti ya mwaka 2018/2019, Serikali na Wizara yetu ya Mifugo tulitenga pesa kwa ajili ya kuweza kuufanyia marekebisho mnada wa Mursagamba na hivi ninavyozungumza, utaratibu wa kuweza kukamilisha hatua hiyo unaendelea na mara tu baada ya kukamilishwa kwa hatua hiyo tutakwenda kuufungua na tutamkaribisha Mheshimiwa Mbunge Gashaza ambae ailipigia debe sana kuhakikisha mnada huu unafunguliwa ili na yeye aweze kushiriki kikamilifu kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu na Wilaya ya Ngara kwa ujumla wake.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika Kijiji cha Mkundi ya Mtae, Tarafa ya Umba ambayo kimsingi Tarafa hii karibu eneo kubwa ni wafugaji, pana migogoro ya ardhi ambayo ni baina ya wakulima na wafugaji na mara kadhaa nimejaribu kuwasiliana na Wizara kuona namna bora ya kutatua mgogoro katika eneo hili ambalo kimsingi eneo hili lilikuwa ni eneo la wafugaji. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuboresha maeneo haya hasa katika sekta nzima ya ufugaji?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imejipanga vyema katika kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji na tumeunda Kamati ambayo inatembea nchi nzima katika kuhakikisha kwamba migogoro ya wakulima na wafugaji inapatiwa suluhu na kwisha kabisa. Kijiji alichokitaja cha Mkundi Mtae ambapo kipo katika Tarafa nzima ya Umba ambayo sisi kama Wizara ya Mifugo tumekitambua kijiji hiki na maeneo mazima ya Tarafa ya Umba kuwa ni maeneo yanayoshughulika zaidi na shughuli za ufugaji. Nataka nimhakikishie Wizara yetu inayo mipango mizuri ya kuhakikisha kwamba fursa na uwekezaji katika mifugo inapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yeye Mwenyewe Mheshimiwa Mbunge Rashid Shangazi ameleta maombi ya kuboresha majosho yaliyoko katika eneo hili. Naomba nimhakikishie kuwa, majosho yale yamechukuliwa na Wizara yetu na yapo katika mpango wa kuhakikisha yanarekebishwa na yatakapokuwa tayari yamerekebishwa sisi katika Wizara tutakuwa pamoja na yeye kwenda nae pale kwenda kuyazindua kwa ajili ya kuboresha sekta yetu ya mifugo.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naomba nimrejeshe Mheshimiwa Naibu Waziri katika swali la msingi la kanuni za ufugaji bora na kilimo cha kisasa. Sasa ni wapi Mheshimiwa Waziri anaweza akatuambia kwamba ni sampling area ambapo Serikali inafanya ufugaji bora na kilimo cha kisasa ambacho kitaondoa hiyo migogoro baina ya wafugaji na wakulima, sampling area katika nchi ni wapi ili wengine wakajifunze?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwanza kwa pongezi zako hizi za kunielekeza kuwa najibu vizuri sana isipokuwa nijibu kwa kifupi na nitafanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Yussuf kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wapi katika nchi? Nataka nimhakikishie tunayo maeneo mengi sana katika nchi ambayo yana wafugaji wanaofuga kisasa katika mikoa mbalimbali. Kwa kuwa amenitaka nijibu kwa mfano sehemu moja tu ambayo Mtanzania au Watanzania wanafanya; ukienda katika Mkoa wa Morogoro utakutana pale na Mfugaji wa kisasa anaitwa Profesa Shemu mwenye ng’ombe zaidi ya 700, ng’ombe wa kisasa wanaozalisha maziwa, huyu ni mmoja wa mfano. Ukienda Wilayani Chato kwa Mheshimiwa…

MWENYEKITI: Inatosha, ahsante.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Moja ya tatizo kubwa linalowakabili wafugaji wa nchi hii hata wakianzisha ufugaji wa kisasa ni upatikanaji wa mbegu bora, lakini mpaka sasa ukifuatulia katika maeneo ambayo kuna artificial insemination ng’ombe waliopo no Borana pamoja na ZEBU wale wa Mpwapwa. Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba inaingiza mbegu bora nchini kwa ajili ya kusaidia wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mfugaji, Mbunge wa Monduli, Mheshimiwa Julius Kalanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango kabambe mzuri sana wa kuhakikisha tunaboresha mbali kwa maana ya kwa safu zetu mifugo katika nchi kwa kusimamia mikakati mikubwa mitatu:-

(i) Wa kwanza ni ule wa artificial insemination ambao umeenea nchi nzima katika vituo vyetu.

(ii) Wa pili ni ule wa kutumia njia ya asili kwa kutumia madume bora ambayo yanapatikana pia katika mashamba yetu. Ukienda katika shamba kama vile la Mabuki-Mwanza, Sao Hill - Iringa na kwingineko tunao Bulls wa kutosha ambao wanaweza kwenda kuboresha mifugo hiyo.

(iii) Ya tatu tunao mpango tunaita “multiple ovulation” ambapo mpango huu unakwenda kukamilika mwaka huu kupitia shamba letu la Mpwapwa ambao huu utakwenda kumaliza kesi hi ya kupatikana kwa mifugo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kalanga na…

MWENYEKITI: Ahsante.
MHE. HAMAD SALIM MAALIM: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, bado nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa Serikali imekubali kuwasaidia wavuvi wadogo wadogo kujikwamua na umasikini na kuleta maendeleo ya Taifa: Je, ni kwa nini basi Serikali hii hii imeamua kuwachomea wavuvi nyavu zao ambazo nyingine hata hazistahiki kuchomwa kama ina lengo hilo?

Swali la pili; kwa kuwa uvuvi si suala la Muungano, lakini uvuvi wa Bahari Kuu ni suala la Muungano, kwa nini basi wavuvi wetu wengi wanaotoka Unguja na Pemba wanaokwenda kuvua katika mpaka wa Tanzania na Kenya wanapokamatwa Serikali yetu inashindwa kuwatetea?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, zoezi la uchomaji nyavu ni zoezi lililokwenda kwa mujibu wa sheria za nchi yetu. Katika kutekeleza zoezi hili la uchomaji nyavu haramu, tumetekeleza kwa kufuata Sheria ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003 lakini na sheria zingine za nchi ikiwemo Sheria ya Mazingira.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wavuvi wote nchini kwamba Serikali iko pamoja nao katika kuhakikisha inawasaidia. Ndiyo maana yapo mambo ambayo tuliyaona kuwa yanafaa kuboreshwa, mathalan katika hili la nyavu, wavuvi wa upande wa bahari ambapo Mheshimiwa Mbunge wa Kojani anatokea, wameleta maombi yao ya kuona kuwa nyavu za milimita 10 siyo nyavu ambazo zinaweza kukamata samaki. Hivyo wametuletea maoni ya kuhakikisha kuwa tunawapelekea nyavu za milimita nane. Sisi kama Serikali tumechukua rai yao na tumeifanyia kazi.

Maboresho ya kanuni hiyo yako tayari, hivi sasa wakati wowote kuanzia sasa matumizi ya nyavu za milimita nane yatatangazwa rasmi ili wavuvi kote nchini hasa wale wa upande wa bahari waweze kunufaika na rasilimali za nchi yetu. Hivyo basi, ningewaomba waendelee kufuata sheria tulizonazo kwa muktadha mzuri wa kulinda rasilimali za Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, ameuliza kuhusiana na Serikali kutokuwasaidia wavuvi wanaokamatwa upande wa kule Mkinga, mpakani na Kenya. Nataka nikuhakikishie na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote na miongoni mwa Wabunge nimashahidi, akiwemo Mheshimiwa Mbunge wa kutoka hukohuko Kojani, Mheshimiwa Kai, tumekuwa tukifanya jitihada nyingi sana, kila mara, wavuvi wetu wanapokamatwa na Serikali yetu kupitia Wizara ya Mambo ya Nje, imekuwa ikifanya mawasiliano na Serikali Kenya, wakati wote, kwa ajili ya kuhakikisha kuwa, wavuvi wale wanaruhusiwa na kupewa dhamana ya kurejea nyumbani kuendelea na shughuli zao. Wakati wote sisi tumekuwa tukiwaomba wavuvi wetu wajielekeze zaidi kuvua katika maeneo ya nchi yetu kwa sababu tunazo rasilimali zakutosha na hatuna sababu ya kwenda kuvua katika maeneo ya nchi nyingine.
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja namajibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza,kwa kuwa hizi bilioni sita alizozisema zimekokotolewa kutoka kwenye net revenue, baada ya kuondoa gharama na kwa kuwa hifadhi ya bahari wanaweka gharama za mafuta, gharama za likizo, gharama za uendeshaji wa hifadhi, mpaka kupelekea gharama zinakuwa ni kubwa lakini net revenue inakuwa ni ndogo ambayo halmashauri ya Mafia inatakiwa ipate asilimia 30.

Sasa swali, je, Mheshimiwa Naibu Waziri, haoni sasa umefika wakati gharama za kukusanya mapato peke yake ndiyo zitolewe, waachane na gharama za uendeshaji wa hifadhi ya bahari kwa sababu gharama zinakuwa ni kubwa na kipato kinakuwa ni kidogo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwamoja ya vikwazo vya Wilaya ya Kisiwa cha Mafia kupata watalii wachache, kwa mwakatunapata pale watalii kama elfu sita, ukilinganisha na Kisiwa cha Zanzibar, moja ya vikwazo ni hii entrance fees ya dola 24 kwa kila mtalii. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri haoni sasa umefika wakati wa kuangalia uwezekano wa kupunguza kiwango hiki cha entrance fees ili kuweza kuvutia watalii wengi kuja katika Kisiwa cha Mafia? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya kaka yangu Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Daukama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza anataka na kutushauri Serikali kuona umuhimu wa kupunguza gharama za uendeshaji ili kusudi ile faida inayopatikana na shughuli nzima za uhifadhi na utalii ziweze kwenda moja kwa moja katika jamii ya Mafia pia. Naomba nimhakikishie kuwa wazo lake hili tunalibeba naSerikalitumelichukua. Kwa kuwa ni jambo la kimchakato, tutakwenda kulitazama na kuona ni namna gani tunavyoweza kuendana na mawazo hayo ya wananchi wa Mafia.

Mheshimiwa Spika,jambo la pili, ni juu yakuona umuhimu wa kupunguza fee ya kuingilia katika maeneo haya ya hifadhi, ili kusudi kupata watalii wengi zaidi. Ni lengo la Serikali la kuhakikisha kuwa watalii wanaongezeka katika maeneo yetu ya utalii na hivyo, kama moja ya kikwazo ni entrance fee, nataka nimhakikishie pia Mheshimiwa Mbunge kwamba, hili nalo ni wazo ambalo tutalichukua, tutakwenda kulikokotoa na kuona umuhimu wake ili kuweza kufikia lengo letu la kuongeza idadi ya watalii nchini.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Serikali, sekta hii ya mifugo bado inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwepo utitiri wa tozo mbalimbali kwa wafugaji ambao karibu ng’ombe moja tozo zake zinazidi shilingi elfu hamsini. Swali la kwanza, je, nini mkakati wa Serikali kuwapunguzia wafugaji tozo hizo ili waweze kuzalisha kwa tija?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, tatizo linalowakabili wafugaji wengi nchini ni pamoja na ugonjwa wa Ndigana Kali ambapo wafugaji tunapoteza zaidi ya asilimia 60 ya ndama wakati wanapozaliwa na chanjo hii bei yake ni shilingi 12,000 kwa ndama. Je, nini mkakati wa Serikali wa kuweka ruzuku au kuondoa kodi katika chanjo hii ili wafugaji waweze kumudu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya mawili ya Mheshimiwa Laizer, Mbunge wa Monduli, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utitiri wa tozo, Wizara imeendelea na utaratibu wa kupitia tozo zote zinazotozwa katika sekta hii ya mifugo na zile zinazoonekana kuwa ni kero kwa wafugaji wetu na wafanyabiashara wa mifugo tumeendelea kuzipunguza. Vilevile zile ambazo zimeonekana kuwa ziko chini tumeendelea kuziongeza kwa manufaa mapana ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili anataka kujua kuhusiana na chanjo. Taasisi yetu ya TVLA na TVI mpaka sasa Tanzania sisi wenyewe tumefanikiwa kutengeneza chanjo tano na chanjo ya Ndigana Kali ni miongoni mwa chanjo tunayoifikiria kuiongezea. Naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili lipo katika mkakati wa Wizara na yenyewe itatengenezwa hapa Tanzania na tutakapofanikiwa itapunguza bei na kuwasaidia wafugaji wetu.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Nakushukuru Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mkoa wa Singida kama ilivyo Monduli ni mabingwa wa kufuga ng’ombe, mbuzi na kondoo.

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuanzisha kiwanda kikubwa cha ngozi na nyama ili kuendana na falsafa ya Tanzania ya Viwanda?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aisharose Matembe, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Singida juu ya kuanzishwa kiwanda cha kuchakata nyama na mazao ya mifugo katika Wilaya ya Manyoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza katika jibu la msingi kwamba Serikali imekuwa na mkakati huo na maeneo mbalimbali katika Taifa letu hivi sasa viwanda vinajengwa. Wazo hili la kujenga pale Manyoni ni jema, naomba tulichukue tulipeleke kwa wawekezaji ili tuweze kupata kiwanda pale Manyoni ambako ni center kwa mifugo inayotoka katika Mkoa wa Kigoma na Mikoa ya Bara kwa maana ya Shinyanga na hata Nzega na Tabora wote wanaweza kupata huduma hii ya kuchakata mifugo kwenye eneo hili kwa kuwa eneo hili ni la kimkakati.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Waziri naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

(i) Kwa kuwa Msitu wa Makele kusini ambao tayari umesha poteza sifa ya uhifadhi, na kwa kuwa tayari yapo maelekezo ya kutoa sehemu ya misitu hii kwa sababu ya wafungaji ili kuondoa usumbufu uliopo kwa nini sasa Serikali isitoe msitu huu wa Makele kusini kwa ajili ya wafugaji?

(ii) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa suala hili la mifugo imekuwa na changamoto kubwa, sambamba na Jimbo la Nyamagada unapozungumzia masuala ya mifugo kwenye minada ya upili watu wana Nyamagana hawana kabisa eneo la kufanyika shughuli zao za uchinjaji na kwa maana mnada. Na kwa sababu na mifugo hii imekuwa inatangatanga mtu anayetoa mfugo Magu lileta Mwanza au anayetoa mfugo Kwimba kuleta Mwanza analazimika kupeleka Misungwi kwenye mnada wa upili ndio arudishe Nyamagana kwa ajili ya uchinjaji au Ilemela na matokeo yake kuongeza gharama za mchinjaji. Ni nini Serikali inatoa kauli gani juu ya minada hii kwa nini usirudishwe pale pale ulipo Nyamgana na watu wakachinja kwa uzuri?
NAIBU WAZIRI MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni juu ya kuomba msitu wa Makele kusini kupewa wafugaji. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Dkt. John Pombe Joseph Magufuli mwaka 2016 alipotembelea katika Mkoa wa Kigoma, alipita katika Wilaya Kasulu na wananchi wa Kasulu walimpa maombi yao ya kuomba msitu huu wa Makele kusini upewe wananchi kwa maana ya shughuli za ufugaji na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alielekeza hekta zipatazo 10,000 zitolewe kwa vijiji viwili 5,000 na 5,000 zigawiwe kwa Halmashuri ya Kasulu. Watendaji wa TFS kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii wametekeleza agizo hili na wananchi wa Kasulu wamepatiwa. Hivi sasa tulichokipendekeza baada ya maelekezo mengine juu ya Rais wetu juu ya kuwapa wafugaji na wakulima maeneo ya ziada kwa ajili shughuli zao tumependekeza eneo la Mkuti katika Wilaya Kasulu na Uvinza ndio sasa yaelekezwe kuangaliwa kama yamepoteza sifa yapewe wafugaji na wakulima. Naomba Mheshimiwa Vuma na wafugaji na wakulima wote katika Wilaya ya Kasulu waendelee kuwa na subra pindi jambo hili litakapokuwa tayari watapata manufaa hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili linahusu minada ya Upili na kwa nini wachinjaji wa pale Mwanza Jiji wanalazimishwa kupeleka mifugo yao katika mnada wa Upili wa Msungwi ndipo waende kuchakata mifugo hiyo pale Mwanza Jiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni urasimu kwa sababu mifugo tumekubaliana ya kwamba minada ya Upili dhumuni lake ni kwa ajili ya wafanyabishara kwa kiwango cha kati na kuwango cha juu. Kwa wale wafanyabishara wadogo wadogo wenye ng’ombe mmoja wawili ama mbuzi mmoja wawili wanaruhusiwa kununua katika minada yao ya misingi na kwenda kuchakata moja kwa moja kwa ajili yakuweza kufanya shughuli hizi za kujipatia kipato na kuhudumia wananchi. Natoa maelekezo kwa watendaji wetu wasimamie sheria kanuni zetu bila kuathiri wananchi wetu na kuinua vipato vyao na kuendeleza maisha yao.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina suala moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mipango mizuri ya Serikali lakini bado wavuvi wana hali ngumu, uduni wa vifaa, utaalam na kadhalika. Je, ni lini Serikali itaanzisha vyuo vya uvuvi vingine kwa sababu navyofahamu chuo kilichopo ni kimoja tu lakini hata wahitimu wake hawapati nafasi ya kuajiriwa pamoja na kwamba tumezungukwa na ukanda mkubwa wa bahari na maziwa. Je, Serikali ina mikakati gani ya kuwatumia wataalam wanaomaliza katika chuo hicho lakini pia kuanzisha vyuo vingine kwa lengo la kuwanyanyua wavuvi ili waweze kuwa na tija na bahari na maziwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili mazuri sana ya nyongeza ya Mama yangu Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali tunao mpango wa kuhakikisha tunafungua vyuo vingine. Hapa karibuni tumefungua chuo cha uvuvi katika Mikoa ya Kusini kwa maana ya Mtwara Mikindani, Chuo cha FETA ambacho kinafanya kazi ya kutoa elimu. Mipango mingine ya Serikali ni pamoja na kuboresha chuo chetu kilichopo pale Pangani maarufu kama KIM kwa kushirikiana na Taasisi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Halmashauri ya Pangani kwa lengo la kuhakikisha wananchi hasa vijana walio wengi wa maeneo haya ya ukanda wa bahari wanapata elimu. Kwa upande wa Ziwa Victoria chuo chetu kilichopo katika Wilaya ya Rorya pale Gabimori na chenyewe tunakwenda kukiongezea nguvu ili kusudi kitoa elimu zaidi kwa wananchi wengi wa maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ameuliza mipango yetu tuliyonayo ya kuhakikisha wale wataalam wanaotoka katika vyuo hivi wanakwenda kupata kazi na kuisaidia jamii yetu. Katika majibu yangu ya msingi nimeeleza kuwa Serikali inao mpango wa kufufua Shirika letu la Uvuvi la TAFICO na tayari tumeshalifufua, hivi sasa tunakwenda katika hatua ya kununua meli. Tayari tumepata msaada kwa maana ya grants kutoka Serikali ya Japan wa takribani bilioni nne ambazo tunakwenda kununua meli na kutengeneza miundombinu ya kuhifadhia samaki katika eneo la ukanda wa pwani. Hii ni chachu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wale wengi wenye utaalam wataajiriwa na mashirika haya.

Vilevile tunao mpango wa kuhakikisha wanajiajiri wao wenyewe kwa kufanya kazi za uvuvi endelevu wa kisasa na vilevile ufugaji wa samaki.
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri ni lini Serikali sasa itahakikisha kwamba bandari ya uvuvi inajengwa ili fursa ya uvuvi wa bahari kuu iweze kutumika vizuri sana? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la ndugu yangu Mbunge wa Mafia, jirani yangu, Mheshimiwa Mbaraka Kitwana Dau, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni lini bandari itajengwa. Hivi sasa tuko katika kumalizia mchakato wa upembuzi yakinifu wa eneo itakapokwenda kujengwa bandari ya uvuvi. Tayari mkandarasi huyu kupitia pesa zetu wenyewe, pesa za ndani tumeshamlipa na anamalizia kazi ya kutuelekeza mahali gani katika ukanda wetu wa pwani tutakwenda kujenga bandari ya uvuvi.

Mheshimiwa Spika, habari njema zaidi, nadhani wote tumemsikia Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alipokuwa katika Mei Mosi pale Mbeya ameeleza juu ya nia njema ya nchi rafiki ya Korea ambapo wameonesha nia ya kutaka kushirikiana nasi katika kwenda kujenga bandari hii ya uvuvi.

Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote na Watanzania kwa ujumla kwamba nia yetu hii itakwenda kutimia na hatimaye kuweza kupata faida ya uvuvi katika eneo la bahari kuu.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa bahati wakati mifugo inahama inakwenda Mkoa wa Lindi Mheshimiwa Naibu Waziri aliyekuwa anajibu alikuwa Mkuu wa Wilaya kule Kilwa na wakati mwingine akikaimu nafasi ya Mkuu wa Mkoa, kwa hiyo, jambo hili analifahamu vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tatizo lililopo ni kwamba, mifugo iliyokuja wakati ule na leo imekuwa mingi kama ime-double kwa hiyo, Mkoa kama wa Lindi umezidiwa na idadi ya mifugo. Swali la msingi Mheshimiwa Mbunge ameuliza kwamba, je, Serikali ipo tayari kuandaa mpango mwingine wa kuhakikisha mifugo ile inapungua kwa sababu, sasa hivi ukataji wa misitu umekuwa mkubwa kulingana na idadi ya mifugo ambayo tunayo? Kwa hiyo, hilo swali la kwanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuna malambo Serikali walijenga katika maeneo haya ya wafugaji, mfano hata pale Jimboni kwangu Mchinga katika eneo la Ktomanga limejengwa lambo kubwa la zaidi ya milioni 300, lakini kwa mwaka wa tatu sasa lambo lile halitumiki kwa sababu tu linahitaji ukarabati wa fedha wa shilingi milioni 22 na kwenye bajeti ya Halmashauri ya mwaka huu ya 19 na 20 tumeomba tupatiwe milioni 22 ili lambo lile lifanyiwe ukarabati na wale wafugaji waweze kupata huduma zao. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari sasa kututhibitishia kwamba, hii milioni 22 wataitoa kwa kuwa ipo kwenye bajeti ili tuweze kutoa huduma kwa wafugaji waliopo maeneo yale? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bobali, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza Mkoa wa Lindi umezidiwa na je, Serikali ina mipango gani ya kuhakikisha kuwa inapunguza mifugo ile iliyozidi pale katika Mkoa wa Lindi. Serikali imefanya jitihada kadhaa, moja ya jitihada ni katika kuhakikisha kwamba, wafugaji wanavuna mifugo yao. Katika kuvuna mifugo hii ni pamoja na ile jitihada ya makusudi ya kuanzisha machinjio za kisasa.

Kwa upande wa Mkoa wa Lindi, Lindi Manispaa imejengwa na inaendelea kujengwa machinjio ya kisasa itakayorahisisha na kuwapa fursa wafugaji wetu waweze kuvuna mifugo yao na kwenda kuiuza katika machinjio ile na hatimaye kuweza kupata faida kwa upande wa wafugaji wenyewe, lakini kwa upande wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali inao mpango madhubuti wa kuhakikisha kuwa inaboresha ufugaji huu, ili kusudi kuweza kufanya ufugaji wenye tija. Ufugaji ambao utamfanya mfugaji awe na mifugo michache, lakini yenye kumpa faida kubwa zaidi kuliko kuwa na makundi makubwa ya mifugo ambayo tija yake wakati mwingine inakuwa ni ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili Mheshimiwa Bobali ameeleza kuwa liko lambo katika Mji wa Mchinga ambalo lambo lile halitumiki na tayari wameshaliweka katika bajeti. Naomba nimhakikishie kuwa, Mheshimiwa Bobali pindi pesa hizi zitakapopatikana sisi kama Serikali tuko tayari kuboresha huduma za mifugo, hivyo, tutalichukua jambo hili na kulitekeleza.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa swali la nyongeza Mkoa wa Njombe ni moja ya Mikoa yenye hali ya hewa nzuri ambayo inaruhusu ng‟ombe wa maziwa kuweza kustawi na kuzalisha maziwa ya kutosha. Je, ni nini Mkakati wa Wizara kuhakikisha kwamba wananchi wa Mkoa wa Njombe ambao wanapenda kufuga wanapata ng‟ombe bora wa kisasa ili uzalishaji uongezeke na pia ili Viwanda viweze kupata malighafi za kutosha? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hongoli kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mkakati wa Serikali katika kuhakikisha tunaongeza idadi ya ng‟ombe katika Mkoa wa Njombe. Majibu ya msingi na majibu ya ziada yaliyojibiwa na Mheshimiwa Waziri yameeleza wazi juu ya Mkakati wa Serikali wa kuongeza idadi ya mitamba katika mashamba yetu ya Serikali likiwemo Shamba la Kitulo lililopo katika Mkoa huo wa Njombe; pia vilevile shamba letu la sao hill lililoko pale Mafinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati hii kwa pamoja, pamoja na mikakati mingine ya kuanzisha makambi ya uhimilishaji wa ng‟ombe mikoani, ambao tunaendelea nao hivi sasa katika maeneo mbalimbali ya hapa nchini ya kuongeza mbali ama breed za kisasa za ng‟ombe watakaotuletea tija zaidi inayokwenda sambasamba na kutuhakikishia kufikia katika lengo la kuwa na ng‟ombe wa maziwa wa kutosha nchini kote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivi sasa tuna takribani ng‟ombe milioni moja wa maziwa wazuri; na mkakati wetu ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2021/2022 tuwe na jumla ya ng‟ombe milioni nne watakao kuwa ng‟ombe wazuri wa maziwa kwa ajili ya uzalishaji mkubwa wa maziwa na kuingiza katika viwanda vyetu.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kujua kwamba Tanzania ni nchi ya pili Afrika kwa ufugaji wa wanyama; ng’ombe, mbuzi, kondoo, punda na mifugo mingine, lakini cha ajabu ni kwamba hatuna kiwanda cha kuchakata mifugo hiyo na sasa hivi Serikali imehamia Dodoma na tuna ranchi ya Kongwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali hili alijibu kwa umakini zaidi, tuna ranchi pale Kongwa. Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba wafugaji wa Dodoma, Shinyanga, Tabora, Mwanza wanaleta mifugo yao Dodoma pale ranchi ya Kongwa, ambapo ombi langu kwa Serikali ni kujengwa kwa kiwanda cha kuchakata mifugo pale Kongwa Ranch ili wananchi wa Mwanza, Shinyanga, Dodoma na Singida wapate mahali pa kuuza mazao ya mifugo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kiwanda cha kuchakata mifugo pale Ruvu kilianza tangu mwaka 2007 na sasa ni miaka 12 kiwanda kile hakijakamilika na fedha nyingi zilishatumika kwa ujenzi wa kiwanda kile; naomba kujua mpango wa Serikali wa kuhakikisha kwamba kile kiwanda cha Ruvu pia kinaanza kazi sambamba na kiwanda kitakachojengwa Kongwa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Tanzania ni nchi ya pili kwa mifugo katika Bara la Afrika. Suala la kutokuwa na kiwanda, naomba tu niliambie Bunge lako Tukufu kwamba tunavyo viwanda katika nchi yetu vinavyochakata mazao ya mifugo, kwa mfano, tunacho kiwanda cha Chobo Investment pale Mwanza kinachomilikiwa na kijana Mtanzania mzalendo ambacho kina uwezo wa kuchakata ng’ombe wasiopungua 500 kwa siku na mbuzi wasipungua 1,000 kwa siku moja. Vile vile tunacho kiwanda cha Serikali hapa hapa Dodoma kinachoitwa TMC.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Bura angependa kuona kuwa viwanda hivi vinachakata mazao ya wafugaji katika Mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Singida na Dodoma. Naomba tu nimhakikishie kuwa kiwanda cha TMC kilichosimama kwa muda kiasi, Serikali imejipanga vyema na tayari tumekirudisha katika utaratibu wa ndani ya mikono ya Serikali kwa lengo la kuhakikisha kiwanda kile kinaendelea na kazi ya kuchinja na kuchakata mifugo ya maeneo haya ya Dodoma, Singida, Shinyanga na Mwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, habari njema zaidi, pale Shinyanga tunacho kiwanda cha siku nyingi zaidi cha Tanganyika Packers ambacho kilichokuliwa na wawekezaji, tumekirudisha pia Serikalini kwa lengo la kuhakikisha kuwa kinaendelea kuchakata mifugo ya wafugaji wetu na kuuza ndani ya nchi na ziada kuweza kuuza nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ni kuhusiana na ujenzi wa kiwanda katika eneo la Ruvu. Kama nilivyojibu katika swali la msingi, ni kwamba NARCO tumeingia ubia na kampuni ya NIKAI ya kutoka Misri ambayo sasa itachukua jukumu hili lote ikiwa ni pamoja na kile kiwanda ambacho tulikianzisha pale mwanzo kuhakikisha kwamba kiwanda hiki kinajengwa kwa pamoja na kuweza kuchinja na kuchakata mazao ya mifugo inayotokana na wafugaji wetu katika Taifa letu.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Njombe Mjini ni wafugaji wa ng’ombe wa maziwa. Tatizo kubwa tunalokabiliwa nalo katika Jimbo la Njombe ni upatikanaji wa ng’ombe bora wa maziwa. Hivi sasa tunapokezana ng’ombe mpaka imefikia mahali sasa ng’ombe wa maziwa anatoa lita moja kiasi ambacho anasababisha hasara kwa wafugaji kwa kuwa hatupati maziwa ya kutosha.

Je, Serikali ina mpango gani sasa kutuwezesha sisi wafugaji wa ng’ombe wa maziwa wa Jimbo la Njombe Mjini kupata ng’ombe bora wa maziwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wetu katika Serikali wa kupatikana kwa ng’ombe bora, tunayo mipango kadhaa ya kuhakikisha tunaongeza idadi ya ng’ombe bora wa maziwa kwa kupitia mfumo wa uhimilishaji (artificial insemination) kwa kuuza mitamba ya kutoka katika mashamba yetu likiwemo shamba la ng’ombe wa maziwa la Kitulo lililoko Makete katika Mkoa huu wa Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachowaomba wafugaji wa Njombe na wafugaji wengine wote nchini wajiunge katika vikundi ili iwe rahisi kuweza kuwasaidia kama tulivyowasaidia kupatikana mitamba ya ng’ombe wa maziwa wafugaji wa Ushirika wa Wafugaji wa Ng’ombe wa Maziwa pale Tanga kwa maana ya Chama Kikuu cha Ushirika cha TDCU ambacho kimepata mkopo kutoka Benki ya Kilimo ya Zaidi ya shilingi bilioni moja na kununua mitamba ya maziwa ya zaidi ya 300 kwa ajili ya kuweza kulisha katika kiwanda cha Tanga Fresh.
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na changamoto za kuelekea Serikali ya viwanda, Mkoa wa Katavi kuna wafugaji wa kutosha, yaani kuna wafugaji wengi katika Jimbo la Mpanda Vijijini, ukienda Jimbo la Kavuu, Inyonga pamoja na Nsibho.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali kupitia Sera ya Serikali ya Viwanda mtafungua kiwanda cha nyama kitakachowezesha kupata mazao ya mifugo kwa maana ya maziwa, ngozi, pamoja na nyama ili wafugaji wa Mkoa wa Katavi wanufaike na Sera hii ya Awamu ya Tano?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mikoa ya Rukwa na Katavi, tunacho kiwanda kizuri sana cha Safi ambacho kimesimama kwa muda mrefu kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kunchela kwamba mchakato ndani ya Serikali unaendelea kung’amua matatizo yote na kuyasuluhisha yaliyokipata kiwanda hiki na kusababisha kutokufanya shughuli zake. Naomba niwahakikishie wana-Katavi na wana-Rukwa wote, baada ya kupatikana kwa utengamano, kiwanda kile kitaendelea kufanya kazi na matokeo yake wafugaji wa Rukwa na Katavi watapeleka mifugo yao pale kwa ajili ya uchakataji na hatimaye kuongeza thamani ya mazao yao.
MHE. JUMA ALI JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwa kuwa Mapato ya Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu yanategemeana na leseni pamoja na vibali kwa meli zinazotoka nje kuvua Tanzania na kwa kuwa 1.4 ndiyo imegoma kuleta meli kutoka nje kuja kuvua hapa: Je, Serikali haioni kwamba huu ni mgogoro wa 0.4?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kama hivyo ndivyo ilivyo, ni lini Serikali itaiondoa hii 0.4 ili tuweze kupata mapato na nchi yetu iweze kusonga mbele? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza katika majibu ya msingi, Serikali ilirekebisha Kanuni na kuweka nyongeza ya vipengele kikiwemo kipengele hiki cha USD 0.4 kwa kilo ya samaki aina ya jodari kwa lengo la kuongeza mapato ya Serikali na kuweza kuinufaisha nchi yetu kutokana na rasilimali hii. Sasa kutokana na changamoto hii aliyoisema ya wateja kutokutokea kwa kugomea hii 0.4, nimeeleza katika jibu la msingi kwamba Serikali iko katika majadiliano ya kutazama juu ya Kanuni hii na baada ya kukubaliana, tutaamua hatua itakayofuata kwa ajili ya maslahi mapana ya Taifa letu.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nikushukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Waziri hebu tueleze Bunge hili, tokea mwaka 2009 sheria hii haijaridhiwa Zanzibar na kutoka Zanzibar kuja Dar es Salaam na kutoka Dar es Salaam kwenda Zanzibar inachukua siku ngapi kutatua tatizo hili? Huu mwaka karibu wa 10; huoni Serikali mnaikosesha mapato kwa jambo ambalo halina msingi wowote?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Spika, katika hii miaka Kumi aliyoitaja Serikali imepata jumla ya Shilingi za Kitanzania Bilioni 22 ambapo mgawanyo wa pesa hizi asilimia 50 huwa inaenda Mamlaka ya Bahari Kuu ambayo ni sawa na Bilioni 11, bilioni Sita ilienda katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Bilioni Nne ilienda katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuridhiwa kwa sheria hii kwa upande wa Zanzibar ni mchakato ambao tunautazama na tunaamini kwamba iko siku moja mchakato huo utakamilika. Kama nilivyosema katika jibu la msingi la awali ya kwamba ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tunafanyia kazi maoni yaliyotolewa na wadau wetu wote juu ya kukwama kwa biashara hii ya Uvuvi wa Bahari Kuu na tunayachakata na hatimae tuweze kutoka na suluhu ya kuhakikisha tunaendelea kuvuna na kulinufaisha Taifa letu.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa fursa ya kuuliza maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jibu la msingi la Mheshimiwa Naibu Waziri limeonesha wavuvi na wadau 520 wamepata elimu hiyo lakini pamoja na kuwapa elimu watu hawa 520 hakuna mfumo rasmi unaoweza kusaidia hii elimu waliyoipata ku-disseminate kuwafikia wadau wengine ambao ni sehemu kubwa ya wakazi wa Jimbo la Ukerewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri mwaka jana alitembelea Jimbo la Buchosa akatumia mfumo mzuri sana kutoa elimu kwa wavuvi wa eneo lile. Swali la kwanza, je, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kuja Ukerewe ili kwa pamoja tushirikiane kuwapa elimu wadau wetu hawa wavuvi waweze kujua hasa nini kinachopaswa kufanyika kwenye eneo la uvuvi kuwaondolea adhabu wanazopata bila kuwa na elimu ya msingi kujua wajibu wao ni upi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, hatua iliyofikiwa na kikundi hiki cha Bugasiga ni nzuri na ilipelekea kupata mkopo wa shilingi milioni 250 na nina kila sababu ya kuipongeza Serikali kuwezesha jambo hili. Changamoto zilizopo ni kwamba mkopo huu unatolewa kwa ushirika unaolazimisha sasa dhamana inayotakiwa iwe ni kwa mtu mmojammoja na matokeo yake sasa mkopo unaonekana kama ni wa mtu mmoja na sio ushirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Serikali kwa nini isitengeneze mfumo kwamba wadau hawa kupitia ushirika wapewe mikopo lakini sasa wao wenyewe waunde SACCOS ili SACCOS zile zikopeshe mdau mmoja mmoja na wawajibike kwa SACCOS halafu SACCOS ndio iwajibike kwenye ushirika? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natoa shukrani kwa Mheshimiwa Mbunge kutupongeza Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kazi nzuri tuliyoifanya katika eneo la Kanda ya Ziwa ya kutoa elimu na akatolea mfano wa Jimbo la Buchosa ambalo hivi sasa tunacho Chama cha Ushirika cha Zilagula Fisheries Cooperative ambacho na chenyewe kimeomba mkopo wa shilingi milioni 300 na kitakwenda kupata kupitia TADB lakini na vyama vingine takribani milioni 50 kila chama shilingi milioni 10. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi la utoaji elimu ni endelevu na sisi Wizara ya Mifugo na Uvuvi tupo tayari tutakwenda Ukerewe mara tu baada ya kuahirishwa kwa Bunge hili kwenda kutoa elimu ile kwa wavuvi wa pale Ukerewe ili waweze kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili linahusu juu ya mfumo wa mikopo kupitia ushirika na SACCOS. Naomba tulichukue wazo lake hili ni ushauri mzuri ambapo Wizara tutaufanyia kazi. Kwa kuwa tayari tunalo Dawati letu la Sekta Binafsi linalofanya kazi nzuri sana ya kuratibu mikopo hii na kuratibu namna ya kuweza kuwasaidia vyama vya ushirika, nataka nimhakikishie kwamba ushauri huu tunauchukua na tunakwenda kuufanyia kazi kwa maslahi mapana ya wadau wetu wa uvuvi ili waweze kusonga mbele. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ambayo kuna wavuvi ni pamoja na Jimbo la Bunda Mjini, wapo wavuvi ambao wanavua kupitia Ziwa Victoria. Hakika vijana wengi wa Jimbo la Bunda Mjini wamehamasika kujiajiri wenyewe kupitia Sekta ya Uvuvi lakini changamoto ni zana za uvuvi nyavu pamoja vitu vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningependa Serikali inijibu ili kuwapa moyo vijana ambao wameamua kujiajiri wenyewe kutokana na uvuvi kupitia Ziwa Victoria, ni lini sasa watawawezesha mitaji ili waweze kuvua kisasa waache ugomvi na DC Bupilipili ambaye anawakamata kila siku?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inayo progamu kama nilivyojibu katika majibu ya msingi ya kuwawezesha wavuvi. Kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, moja ya jambo ambalo tuliligundua ni kwamba wavuvi na hata wafugaji wetu hawakopesheki. Ndiyo maana vijana wengi wanaojihusisha na shughuli hizi wamekosa fursa ya kuweza kupata mikopo na hatimaye kuweza kuboresha shughuli zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu kubwa za kukosa mikopo zipo mbili; ya kwanza mabenki yanataka dhamana na pili ni bima kwa maana shughuli za mifugo na uvuvi hazina bima. Nataka niwahakikishie Wabunge wote wa Bunge hili Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzana, Wizara imefanya kazi nzuri na sasa mabenki yametukubalia.

Naomba nitoe shukrani zangu za dhati kwa Benki ya Posta Tanzania imefungua na kuanzisha Akaunti Maalum ya Wavuvi (Wavuvi Account) yenye lengo mahsusi la kuweza kuwasaidia kwa unafuu sana wavuvi wote. Kwa hiyo, nitawaelekeza Benki ya Posta waje pale Bunda Mjini waweze kuwapata vijana na waweze kushirikiana nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili la pili la dhamana, tumefanya kazi kubwa ya kuhakikisha tunalishawishi Shrika letu la Bima la Taifa na limekubali mwezi huu wa pili tutasaini nao mkataba maalum utakaowawezesha sasa kuwa na bima ya mifugo na uvuvi. Hii itakuwa ni hatua kubwa sana kuelekea katika kuhakikisha wavuvi na wafugaji wetu wote wanaweza kupata mikopo katika benki kama vile ambavyo wanaweza kupata Watanzania wengine baada ya kuwa na uhakika wa dhamana na bima.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nina maswali mawili madogo kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, Mheshimiwa Naibu Waziri ametuambia kwamba kila upande wa Muungano una sheria, kanuni na miongozo yake ya shughuli za uvuvi lakini wakati huohuo wavuvi wetu wanaotoka Zanzibar kuja kuvua huu upande wa pili wa Tanzania Bara maeneo ya Bagamoyo, Tanga na maeneo mengine baadhi ya maeneo wanatozwa tozo ya Sh.10,000 hasa pale Tanga askari wa Marine Park wanalazimisha kutoa tozo hiyo kwa mwezi kwa kila mvuvi. Je, hiyo ni sheria, kanuni ama miongozo kuwatoza tozo ndugu zenu wa damu wa Zanzibar ya Shilingi 10,000? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Masoud, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, wavuvi wanaotoka upande wa Tanzania Visiwani kuja Tanzania Bara katika mwambao na wanatozwa tozo mbalimbali. Ameuliza maswali hapo akitaka kujua hizi tozo zipo kwa mujibu, moja, wa sheria; mbili, wa kanuni; tatu, miongozo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa jambo hili laweza kuwa ni geni, naomba tu nichukue hoja hii ya Mheshimiwa Mbunge. Nataka nimhakikishie kwa sababu ameitaja Marine Park and Reserve Unit ambayo iko ndani ya Wizara yangu, nitalifuatilia kutaka kujua uhalali na inatozwa kama alivyouliza katika maswali yake hayo matatu kwa mujibu wa ama sheria, kanuni au mwongozo gani. Ahsante sana.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nimesikia jawabu la Serikali, lakini yeye amejibu mabomu hakujibu gesi. Gesi katika kuzamia haina madhara yoyote kwa sababu kwenye kina kirefu cha maji wenyewe tunaita bahari lujii inawezekana ikawa watu wanatumia nyavu kwa hiyo nyavu imekwama kule chini, kwa sababu ni kina kirefu anaweza akatumia gesi kuzamia kwenda kule. Halafu kingine, hayo mazingira ambayo anayasema Mheshimiwa Waziri kwamba yanaweza yakaharibiwa kwa mabomu kwa baharini wakati mwingine maji yanakupwa yanaweza yakafikika hata kwa miguu lakini haja ya gesi inakuwepo pale maji yanapojaa.

Mheshimiwa Spika, naomba Waziri azidi kuniambia chupa inaharibu kitu gani alichotaja hapa ni mabomu, chupa inaharibu kitu gani, mabomu yanaweza yakategwa hata bila ya chupa. Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Hassan King, Mbunge wa Jang’ombe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi nimeeleza kwamba ugomvi wetu siyo chupa, ugomvi ni matumizi yanayotokana na ile mitungi ya gesi. Kwa maana tunafahamu kuna mahali katika bahari umbali kwa maana ya kina kilomita 40, mvuvi ni lazima awe na namna ya kuweza kumfikisha kule na kufanya shughuli yake, lakini kwa utafiti wetu hapo nyuma ilionekana wazi kwamba waliokuwa wakienda kufanya uzamiaji, ukiacha wale waliofanya uzamiaji kwa ajili ya sport fishing na utafiti, wengine wote walikuwa ni wale wanaoambatana na shughuli za uvuvi haramu na ndiyo maana Serikali ikasema kwa sababu hiyo basi tutazuia zoezi hili isipokuwa kwa kibali maalum cha wale wanaofanya utafiti na wale wanaofanya sport fishing.

Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba kwa sasa Serikali tupo katika kuboresha sheria zetu na kuboresha kanuni zetu, tumekisikia kilio hiki cha wavuvi wazamiaji na sisi tunakifanyia kazi, endapo sheria hizi zitapitishwa na kanuni hizi mpya tuna imani kwamba inawezekana katika jambo ambalo litakuwa limekwenda kuboreshwa mojawapo ni jambo hili. (Makofi)
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kuuliza swali moja la nyongeza. Kumekuwa na mkanganyiko mkubwa sana baina ya zana zipi zinaweza kutumika katika uvuvi na zipi hazifai. Miongoni mwa maeneo ambayo mkanganyiko huo upo ni pamoja na katika Jimbo langu la Mtwara na mara nyingi tumekuwa tukimwomba Waziri au Naibu Waziri mwenyewe waje ili wakae na wavuvi wakubaliane kipi ni sahihi na kipi si sahihi lakini suala hilo limekuwa gumu. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuniambia ni lini atakuja Mtwara ili kuongea na wavuvi wa Mtwara kwa sababu kwa zaidi ya miaka mitatu hawajawahi kumwona Waziri wala Naibu Waziri?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Ghasia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza kwa kufuatilia kwa karibu sana hali za wavuvi wa Mtwara na naomba tu nimhakikishie kwamba Serikali iko makini sana katika kuwafuatilia wavuvi wetu.

Mheshimiwa Spika, nimefika Mtwara, nimefanya mkutano na wavuvi wa Mtwara katika Mji wa Mikindani katika Chuo tulichokijenga cha Wavuvi cha FETA ambako ni mji wa asili wa kwake yeye mwenyewe Mheshimiwa Hawa Ghasia. Nataka nimwambie kwamba nilikutana na wavuvi na nikazungumza nao mwaka jana na katika kesi walizonipatia moja ya kesi ni matumizi ya zana aina ya nyavu za ring net, mgogoro wao ni muda gani utumike mtando huu kwa maana ya mtego huu wa ring net na ugomvi wao ni kina cha kutumika kwa zana hii ya ring net.
Naomba nimhakikishie kuwa katika jambo lingine lililotokea pale Mikindani ni choo ambacho wavuvi walikilalamikia cha pale sokoni ambacho tulitoa maelekezo kwa Halmashauri waweze kukirekebisha na taarifa tuliyonayo ni kwamba tayari wameshafanya marekebisho hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa hii dhana ya kutumia kutokana na kina wavuvi walio wengi wangependa sana kuona wanatumia zana hizi nje maji mepesi, maji mafupi ambapo kwa kufanya hivyo wanakwenda katika uharibifu wa mazingira ya bahari kwa sababu huku katika maji mafupi, ndiko samaki wanakozaliana na wanapokuja kuweka nyavu zile maana yake ni kwamba wanaharibu maeneo ya mazalia. Naomba nimhakikishie kwamba nitarudi tena Mtwara kwenda kuzungumza na wavuvi na kuweza kupata hatima ya shughuli zao.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Wavuvi wengi walikuwa wanategemea uvuvi wa jongoo bahari kuendesha maisha yao na jongoo bahari ni dhahabu ya baharini. Jongoo bahari sasa hivi anafikia dola 30 kwa kilo moja, lakini Serikali imepiga marufuku uvuvi wa jongoo bahari, tunataka kujua kuna faida gani Serikali inapata kwa kupiga marufuku ya uvuvi wa jongoo bahari hali wananchi wanaathirika kwa kukosa mapato?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa fursa hii ya kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Khatibu, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ni kweli miaka ya hapa karibuni, ilipiga marufuku uvuvi wa majongoo bahari. Majongoo bahari ni miongoni mwa viumbe vilivyokuwa vinatishiwa kutoweka, kwa hivyo kwa kulinda rasilimali hii Serikali ikapiga marufuku katika eneo lote la pwani ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, hapa karibuni kama anavyothibitisha Mheshimiwa Khatib na ni kweli, jongoo bahari ni mali na ni mali sana tumeliona jambo hilo na tumeiona fursa hiyo. Mkakati wetu ni kuhakikisha kwamba wananchi walio wengi siyo tu kusubiri majongoo bahari yale ya asili kwa maana wild animals, sasa tunakwenda katika utaratibu wa kuwafuga pia kwa maana ya mariculture. Tunataka fursa hii ienee katika ukanda wote wa pwani tutafuga majongoo bahari, tutainua mwani, tutainua pia vile vile na mazao mengine ikiwemo kaa ambao wenzetu katika Mataifa mengine kama Uchina wanapenda na wanataka sana. Kwa hivyo Waheshimiwa Wabunge wale wa pwani wakae mkao wa utayari wa kupokea fursa hizi na tuwahamasishe Watanzania wavuvi wa pwani wakae katika vikundi ambavyo vitatusaidia kuwapelekea fursa hii kwa urahisi zaidi.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, ukatili mkubwa wa Wanyama unafanywa pindi Wanyama wanaposafirishwa, tumeshuhudia malori yakipita matani na matani yanatoa ng’ombe Karagwe Kanda ya Ziwa yanapeleka Dar es Salaama.

Mheshimiwa Spika, Sasa kwa nini Serikali isitoe agizo ijengwe Kiwanda huko, ng’ombe zichinjwe ndiyo wasafirishwe wapelekwe Dar es Salaam? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Swali la pili, ukatili mbaya kuliko wote ni upigaji chapa wa ng’ombe, tumeshuhudia ng’ombe wakiteswa kwa kupigwa chapa, Serikali imeshindwa kubuni mbinu nyingine tofauti na hiyo, Je, Serikali inatoa kauli gani na upigaji chapa wa hovyo kabisa na utesaji wa mifugo yetu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, dhamira ya Serikali ni kuhakikisha tunajenga Viwanda vya kutosha vya kuchakata mazao ya mifugo, na ndiyo maana katika baadhi ambapo mifugo inapatikana kwa wingi kama vile Mkoani Arusha katika Wilaya ya Longido tumefanikiwa kujenga Kiwanda ambacho kipo katika hatua nzuri ya kumalizika na hatimaye kuweza kuchakata mifugo.

Mheshimiwa Spika, rai yake ni kwa nini tusafirishe mifugo kutoka Karagwe na Mikoa mingine kama Kigoma na kupeleka katika machinjio, hali ambayo inapelekea kurundikana kwa mifugo katika magari na hatimaye kuitesa mifugo hiyo. Sisi tutaendelea na jitihada ya kuhakikisha mpaka kule Karagwe Kigoma na kwingineko Viwanda hivi vinaenea. Lakini ndiyo maana Serikali inaendelea kuboresha pia vilevile miundombinu yetu ili kusudi hata hizi hali za ukusanyaji wa mifugo kwa wingi katika magari wakati mwingine ni kwa sababu ya miundombinu.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Mkoa wa Kigoma, ile harakati ya ujenzi wa barabara ile, itarahisisha mifugo inayotoka katika Mkoa huo ili iweze kufika katika soko na hatimaye kuwanufaisha wafugaji na wananchi wa Mikoa hii ambayo ina mifugo kwa wingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ni suala la upigaji chapa ng’ombe, kwanza naomba nilieleze Bunge lako Tukufu kuwa tunayo Sheria mahsusi kabisa ya utambuzi wa Wanyama katika Sheria za nchi yetu. Sheria hii inatuelekeza kila ng’ombe lazima atambuliwe na hii ni katika kuhakikisha kuwa tunakwenda sambasamba na mahitaji ya Sheria za Kimataifa ya soko la Kimataifa na nyingenezo.

Mheshimiwa Spika, rai yake ni kwa nini tusitafute njia nyingine mbadala, badala ya kuchoma ng’ombe moto, rai hii ya Waheshimiwa Wabunge tunaichukua na tumeanza kufanya kazi ya kuhakikisha tunatumia teknolojia ya hereni, earrings kwa upande wa ng’ombe wa maziwa, kwa kuwa Wabunge wengi wanaonekana kuwa wangependa kuona tunabadilisha utaratibu huu wa kuchoma moto tumelichukua jambo hili na tutalifanyia kazi kwa ajili ya kuweza kuitekeleza vyema Sheria ile ya utambuzi wa mifugo yetu.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, ukatili wa Wanyama uko katika jamii zetu, hususani pale kwenye masuala ya migogoro unapokuta hifadhi na wanaovamia hifadhi, basi Wanyama wale unakuta wanapigwa risasi ama wanakatwa mapanga, na pia tunauona ukatili huu katika usafirishaji unapokuta idadi kubwa ya Wanyama hawa wakisafirishwa kwa masafa marefu na wakiwa wamebanwa sana katika yale magari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitendo hata cha kuwapandisha kwenye yale magari na kuwashusha ng’ombe wale au Wanyama wale wanakuwa wanapigwa, sasa Serikali inajipangaje katika kusimamia hili kimatendo kwamba dhuluma hizi na ukatili huu kwa Wanyama unakuwa umeisha, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ni juu ya ukatili unaofanywa wakati mifugo inapokuwa imekamatwa, katika hifadhi na maeneo mengine, Wizara imeliona jambo hili na nataka nilihakikishie Bunge kuwa Sheria ipo ya haki za Wanyama. Mfugo unapokamatwa, unazo haki zake lazima wapate maji, lazima wapate malisho na watazamwe na hata ikiwezekana wapate na chanjo pia vilevile.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukiwasisitiza wale wote wanaokamata mifugo waweze kutekeleza matakwa haya ya Sheria lakini kwa kukazia, tumeona kwa safari hii tunakwenda kuiboresha zaidi Sheria yetu ya Mifugo ya haki za Wanyama, ili hawa wanaokamata kiholela holela ni lazima wahakikishe kuwa siyo kila mtu anaweza akakamata tu anavyojisikia kukamata.

Mheshimiwa Spika, ni lazima watu wetu wanaohusika na tasnia ya haki za Wanyama, kwa maana ya Maafisa Mifugo kote nchini, waweze kushirikishwa, ili haki za Wanyama wale ziweze kutekelezwa ipasavyo, na jambo la pili ni hili linalohusu mrundikano katika magari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba jambo hili linafanywa sana, na wafanyabiashara wetu, lakini labda nikueleze jambo moja na nilieleze Bunge lako Tukufu wafanyabiashara wale huwa tunawasimamisha katika magari, na wakati mwingine tunawauliza kwa nini mnawarundika ng’ombe namna hii, sasa majibu yao ya haraka ambayo watakujibu ni kwamba ng’ombe ukiwaacha bila ya kusimama wakawa wameshikana hivi, mmoja akikaa chini, mathalani, ng’ombe huyo hawezi kufika salama anapokwenda ni lazima atakufa, kwa sababu ya kukanyagwa na wenzake.

Mheshimiwa Spika, sasa haya yote tumeyaona na ndiyo maana tukasema kwamba ni muhimu tuweze kuirekebisha ile Sheria. Na ndiyo maana unaweza ukaona wakati mmoja tulipoona kuwa ng’ombe hawa wanajazwa sana Sheria yetu ya barabara ilileta kidogo sintofahamu miongoni mwa wafanyabiashara wa ng’ombe kwa sababu walitakiwa wahakikishe wale ng’ombe wanapokuwa kwenye magari wasitingishike.

Mheshimiwa Spika, na maana yake wanapotingishika, katika Sheria inaleta tabu kwa upande wa ulinzi wa miundombinu yetu, na hili wamefanya kwa sababu wasitingishike kwa kuona kuwa wanawekwa wengi, sasa unaweza ukaona kwamba tunao wajibu kweli kabisa wa kuangalia Sheria zetu na kuziboresha na naomba niliahidi Bunge lako kwamba hili tunalifanyia kazi na tunatoa wito kwa wale wote wanaosafirisha mifugo wazingatie haki za Mifugo, na siyo kuwapeleka katika uholela.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri sana, juu ya hili suala la ukamataji holela wa Mifugo na jinsi kama Mheshimiwa Mbunge alivyoliuliza.

Mheshimiwa Spika, nataka kuongezea tu kwamba kwa hivi karibuni baadhi ya Watendaji wa Serikali wamekuwa wakiwaona hata Mifugo na wenyewe ni wahalifu, hawa ni viumbe hai wana mahitaji yao ya msingi ya maji, wana mahitaji yao ya msingi ya malisho, wana mahitaji yao ya msingi ya chanjo na tiba.

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo, hata wanapokamatwa si wahalifu katika namna yoyote katika makosa yoyote ambayo yanamuhusu mmliki wa mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo baada ya kuona hivyo kwamba ukamataji sasa kila Afisa wa Serikali anakamata Mifugo tukaamua kama alivyosema Naibu Waziri kuboresha Kanuni za Sheria ya Ustawi wa Wanyama Na. 19 ya mwaka 2008 na Sheria ya magonjwa ya Mifugo Na. 17 ya mwaka 2003, ambapo marekebisho ya Kanuni ya hizi, yatakuwa tayari ifikapo tarehe 01 mwezi wa saba, ili kuweza kushughulika na hawa Watendaji wa Serikali ambao wamegeuza wameleta manyanyaso makubwa sana kwa Mifugo na Mifugo mingi imekuwa ikifa, ikiwa imeshikiliwa kwa sababu zisizojulikana. Lakini vilevile, kuwaeleza Watanzania wajue kwamba katika raslimali za Taifa, Mifugo ni raslimali ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa vyovyote vile unapofanya, vyovyote vile unavyofanya unaharibu kama Mifugo ikifa ikiwa imeshikiliwa maana yake kwamba raslimali ya Taifa imekufa ikiwa imeshikiliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, suala hili tunalifanya kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba ifikapo tarehe 1 mwezi wa saba, hawa tutashukughulika nao, Watendaji ambao wamekuwa wakitoa kisingizio cha kwamba, natekeleza Sheria anasahau kwamba hata mifugo hawa nao wana Sheria zao zinazowalinda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hatutakubali tena kama Serikali ifikapo tarehe moja mwezi wa saba badala ya huyu Afisa ambaye anasema kwamba anatumia mgongo wa Sheria tutawashughulikia wao kama individual na wala siyo Serikali tena. (Makofi)
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya kutoka Wizarani kwanza nianze kwa kumkumbusha kwamba naitwa Maria Ndila Kangoye siyo kama hivyo alivyonitaja. Nitauliza swali moja la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, Tanzania ni kati ya Nchi zinazoongoza katika ufugaji Barani Afrika hususani ufugaji wa Ng’ombe, lakini licha ya hivyo tumekuwa nyuma sana katika biashara ya mazao ya mifugo. Ningependa kujua ni nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba inakabiliana na upungufu mkubwa wa viwanda vya kuchakata nyama na maziwa nchini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la nyongeza pamoja pia na kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa na mkakati mkubwa na mzuri sana wa kuhakikisha tunapata viwanda vya uchakataji wa mifugo Nchini. Kwa kuanzia kwa haraka haraka hivi sasa, tunavyo viwanda takribani vitatu tunavyovijenga katika Nchi. Kiko kiwanda pale Mkoani Arusha, Wilayani Longido, tunacho kiwanda pale Mkoani Pwani katika Wilaya ya KIbaha, tuna kiwanda kikubwa ambacho tunakitarajia tulichoingia mkataba na Taifa la Misri kitakachojengwa katika Ranch yetu ya Ruvu pale Kibaha pia. Sambamba na kuchakata nyama, tunavyo viwanda ambavyo vinachakata mazao mengine ya mifugo kama vile maziwa.

Mheshimiwa Soika, Serikali inaendelea kuhamasisha sekta binafsi katika kuwekeza kwenye viwanda na mazingira ya uwekezaji katika viwanda hivi vya uchakataji wa mifugo yako mazuri na tunawakaribisha kwa ajili ya kufanya kazi hii.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri swali hili umepewa siku nyingi na hili swali limeuliza ni lini na ni wapi, umejibu kwa ujumla naomba nifahamu hivyo viwanda vitano vya kuchakata samaki katika ukanda wa Pwani viko maeneo gani, kama na sisi watu wa Mtwara vinatuhusu vipo huko kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upembuzi yakinifu wa ujenzi wa bandari umesema utakapokamilika, nataka uwe specific unakamilika lini ili hiyo bandari ipatikane kwa maendeleo ya wavuvi na nchi yetu kwa ujumla, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ni wapi viwanda hivyo vipo; viwanda hivyo katika Mkoa wa Dar es salaam, Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Tanga. Mkoa wa Dar es salaam tunacho kiwanda cha Alfa Cluster, Bahari Food, Pugu Road lakini vilevile Mkoa wa Pwani tunacho Kiwanda cha Abajuko kilichopo pale Vikindu Madafu, Mkuranga na vilevile tunacho kiwanda cha Alfa Cluster, Tanga Jiji ambacho kinafanya kazi ya kuchakata samaki aina ya pweza.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, ni lini hasa tutamaliza hii kazi ya upembuzi yakinifu ya ujenzi wa bandari ya uvuvi, tutamaliza. Mkandarasi amepewa muda wa mwaka mmoja kwa hivyo bado yupo ndani ya muda wa kukamilisha kazi yake na hatimaye atuletee ile ripoti ambayo itakuwa na ushauri wa mahala kuzuri zaidi tutakapoweza kuweka bandari yetu lakini na gharama zake za ujenzi wa ile bandari yenyewe. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa hapa amebainisha wazi kwamba kitambi kinasababishwa zaidi na vyakula vilivyopitiliza hasa vyenye wanga na kwa tamaduni zetu watanzania karibia vyakula vyote tunavyovitumia ni vya wanga. Je, Serikali inatushauri watanzania tule vyakula gani ili kuepukana na vitambi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, utakuwa ni shahidi kwamba sasa hivi kuna ongezeko kubwa sana la uzito uliopitiliza kwa watoto, vijana lakini hata kwa akinamama na hapa tunapozungumza hivyo vitambi pia hata kina mama wanavyo. Sasa tunataka tuone kwamba Serikali ina mkakati gani mahususi, hapa wamezungumzia habari ya chanjo lakini pamoja na hizo elimu wanazotoa, ni nini kifanyike ili tatizo hili lisiendelee kuathiri haswa malika haya madogo ambayo nimeyataja? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, wanga kwa nini ndiyo unaosababisha na Serikali ina ushauri gani? Kwa ruksa yako naomba niwakumbushe hatua za kibailojia kidogo Waheshimiwa Wabunge, wanga ni mzuri kwa mwili, lakini kazi ya wanga ni kuzalisha nguvu tu, unapoliwa ukapitiliza kwa wale ambao mnakumbuka somo ya biolojia wanga uliozidi unageuzwa kwenda kuwa complex compound inayoitwa glycogen haya ni mafuta. (Makofi)

Mheshimwia Spika, sasa glycogen katika mwili wa binadamu hasa mtu mzima hauna kazi nyingine yoyote isipokuwa ni kuhifadhiwa, na huu hii glycogen ambayo kiasili ni protini inahifadhiwa katika maeneo mbalimbali ya mwili wa binadamu ikiwa ni pamoja na mishipa ya kupitisha damu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana tunasema pamoja na appetite ambayo inaweza kukufanya ule ugali mwingi sana, lakini ni vizuri ukala kiasi kile ambacho kitakwenda kuzalisha energy kwa maana ya nguvu ya kuusukuma ule mwili wenyewe, unapokula ziada ndiyo huleta matatizo.

Sasa sisi ushauri wetu kama Serikali nini, kwanza ni kula ulaji ambao unazingatia mlo wenye tunaita mlo bora na hasa protini na katika upande wa protini pamoja na ubora wote wa protini za nyama, lakini protini iliyo bora zaidi ni ile protini inayotokana na mimea. Ushauri wetu Waheshimiwa Wabunge mle zaidi protini na hasa protini zinazotokana na mimea.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili Mheshimiwa Mbunge Rashid Shangazi anauliza nini kifanyike ili hili rika ambalo linaonekana linaathirika zaidi kama vile vijana na hata wakinamama amewataja. Sisi Serikali tunashauri, kwa kawaida kisayansi inakubalika kwa watu wazima kuwa ndiyo waathirika zaidi wa upatikanaji wa vitambi, wanapopata vijana ni jambo lisilokuwa la kawaida. Sasa vijana wanachoshauriwa ni kubadilisha lifestyle namna ya uendaji katika maisha, ulaji wa chipsi uliopitiliza, na unywaji wa pombe uliopitiliza haya ndiyo yanayopelekea matatizo haya…

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Naibu Waziri.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, lakini na ufanyaji wa mazoei pia, ninashukuru.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niiulize wali dogo la nyongeza. Kwanza nimpongeze sana mdogo wangu Ulega inaonekana shuleni alifanya vizuri kwenye somo la biolojia, na ni mfano mzuri nimefuata ule ushari wake ndiyo maana kitambi changu kimepungua. Serikali inajitahidi kupambana na magonjwa mbalimbali nchini hivi karibuni kuna ugonjwa wa homa ya Dengue ambao hali yake sasa ni mbaya na vimeanza kuripotiwa vifo kutokana na jambo hili. (Makofi)

Sasa Serikali inachukua hatua gani kwa kuhakikisha jambo hili linakwisha kwa sababu tukiendelea kulinyamazia vifo vitaendelea kuongezeka watu wanaendelea kumwa na hali ya Jiji la Dar es Salaam kwa sasa ni mbaya?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nape Moses Nnauye Mbunge wa Mtama kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa hapa karibuni imeibuka ugonjwa wa Dengue na hasa katika Jiji la Dar es Salam, Serikali inafahamu juu ya tatizo hili na imeanza kuchukua hatua za makusudi.

Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote na watanzania. Moja katika jambo kubwa ililoligundua Serikali ni kuwa gharama kubwa zinazolipwa na watanzania wanaopata matatizo hayo katika sehemu za kutolea huduma za afya. Sasa katika Serikali jitihada inayofanyika hivi sasa ni kuhakikisha matibabu ya Dengue yanakuwepo na yanapatikana kwa bei zilizokuwa nafuu ili kuweza kuwasaidia watanzania. (Makofi)
MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante, mara nyingi tunaambiwa kwamba wale wanaotaka kupunguza mwili ama vitambi wanakatazwa kula aina ya nyama na badala yake wanaelekezwa kula samaki na nyama za kuku, lakini katika hizi nyama za kuku kuna hawa makuku kutoka nje ambao kama yanauzwa kama KFC ambayo yanamapaja kama watu, Mheshimiwa hebu tunataka ushahidi juu ya kuku hawa wa kizungu broilers hasa katika kuongeza vitambi. (Kicheko)

Je, hawana mahusiano ya moja kwa moja kuku hawa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ulaji wa kuku broilers kwanza kuku ni katika protini na nimesema na nimesema katika jibu la msingi kuwa protini ni muhimu, protini ziko za aina inyotokana na wanyama na ile protini inayotokana na mimea. Lakini anataka uhakika ya kwamba broilers wanatatizo hilo la kuweza kumfanya mtu awe na kitambi au laa!

Mheshimiwa Spika, hakuna utafiti wa kisayansi unaokwenda kutupelekea kutuambia kuwa broilers wanashida katika afya ya wanadamu, jambo hili liko palepale, ulaji wa kupitiliza unaweza kukupelekea katika hayo matatizo. Lakini naomba niwahakikishie broilers hawana shida yoyote, kinachowafanya broilers wakue ni hormones, ambazo hormones kisayansi ni vitamins. Kwa hivyo sisi wanasayansi tunachokifanya vyakula vya broilers tunaweka vitamins za kutosheleza za kuhakikisha ukuaji wao unakuwa ni ukuaji wa haraka…

SPIKA: Ahsante sana.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kulinganisha na kuku wa kienyeji.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi niulize swali langu. Nilikuwa napenda kuiuliza Serikali kwamba sisi tusiokuwa na vitambi tunakula vyakula vyote hivyo ambavyo Mheshimiwa Dkt. Ulega amevizungumza na hatujawahi kuona mabadiliko yoyote katika maumbile yetu. Je, Serikali inatushauri tule nini zaidi kwa sababu vya wanga, vinywaji vyote tumetumia bado tuko kwenye maumbile haya haya.

Je, Serikali inatushauri tule nini ili na sisi tubadilike tufanane na wao? (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nataka kujua watu wa aina yake ambao miili yao haina shukurani kama ulivyoiita wafanyeje? Na yeye anataka kupata kitambi, namshauri Mheshimiwa Musukuma na yeye ikiwezekana apate kuwaona watalaam wa lishe nina hakika watampangia diet ambayo itampelekea na yeye kupata mwili anaouhitaji.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nitaenda kwenye swali la msingi kuhusu non committable disease, 2016/2020 ulitengenezwa mkakati maalum kuhusiana na magonjwa yasiyokuwa ya kuambukizwa.

Je, mkakati huu wamagonjwa yasiyokuwa ya kuambukiza ulikuwa ni kwa nchi nzima au ulikuwa ni pilot project? Na kama ni pilot project kwa maeneo gani?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, mkakati ulikuwa ni pilot ama ulikuwa ni wan chi nzima. Utafiti kwa kawaida huwa ni pilot unachukuliwa eneo moja halafu kwa njia labda kama ya sampling kisha matokeo yanatokana na eneo lile yanaweza kuwa ndio matokeo elekezi. Kwa hivyo naomba nimuhakikishie mama yangu kuwa kwa maelezo ziada ya matokeo ya utafiti huu uliofanywa niko tayari baada ya Bunge kuweza kuzungumza na wataalam wetu na kumtafutia zile takwimu na kuweza kumpatia.
MHE. MACHANO OTHMAN SAID: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na pia nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake. Pamoja na majibu yake, naomba kuuliza swali moja la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wananchi wengi wa Zanzibar shughuli zao ni uvuvi; na kwa kuwa biashara ya dagaa ni kubwa sana kwa Zanzibar na soko lake kubwa ni Congo (DRC) na Rwanda. Ni sababu gani inasababisha kila tani moja ya dagaa kutozwa dola 400 katika mpaka wa Tunduma?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Machano, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nimemsikia vyema amezungumzia na kutaka kujua juu ya mgogoro wa usafirishaji wa mazao ya uvuvi (dagaa) kutoka Tanzania aidha Visiwani na Bara kwenda nje ya nchi na inaonekana tozo ni kubwa na wafanyabiashara kuishindwa kulipa tozo hiyo.

Mheshimiwa Spika, hapa karibuni Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi tulifanya mabadiliko ya tozo mbalimbali za mazao yetu ya mifugo na uvuvi. Tozo zile tulizoziweka zimepelekea wafanyabiashara hasa wa Ukanda wa Pwani kuwa juu ya uwezo wao. Baada ya malalamiko makubwa, Wizara imeyapokea malalamiko yao, imeyafanyia kazi na tumefanya marekebisho ya tozo zile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya bajeti ya Wizara ya Fedha na tozo mpya kupitishwa na Serikali na kutangazwa katika Gazeti la Serikali, kuanzia tarehe 1 Julai, tunayo matumaini kwamba tozo zile zitashuka sana na wafanyabiashara wataendelea kutoa mazao yale ya mifugo kupeleka katika nchi zingine zinazohitaji. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge na wafanyabiashara wote wawe na subra muda si mrefu majibu ya jambo hili yatakuwa yamepatikana.
MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu swali langu vizuri kabisa na nakiri kabisa kwamba asilimia 99 ya walipuaji wa mabomu umefikia. Juhudi hizi nakumbuka Mheshimiwa Naibu Waziri alivyokuwa Mbunge, alivyokuwa Mkuu wa Wilaya kule Kilwa tulishirikiana na mimi kutembea Wilaya ya Kilwa nzima kuelimisha ulinzi shirikishi wa BMU na matokeo yake BMU ndiyo imesababisha kupungua kwa milipuko hii.

Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi hizo kuna viongozi wa Wilaya ya Kilwa, Diwani wa Kata ya Kivinje na DAS wa Wilaya ya Kilwa wanawafuatalia sana hawa viongozi wa BMU na kufikia hatua ya kuwashtaki kwa kutekeleza jambo hili la kusimamia BMU kwa uhakika na wakafikishwa mahakamani, lakini Mwenyezi Mungu wakashinda kesi.

SPIKA: Uliza swali lako sasa Mheshimiwa Bungara.

MHE. SULEMAN S. BUNGARA: Je, hauoni hawa viongozi wa Wilaya ya Kilwa wanawakatisha tamaa wananchi wa Kilwa? Moja hiyo.

Mheshimiwa Spika, pili katika Operesheni Jodari wananchi wa Kilwa walichomewa moto nyavu zao nyingi sana, lakini kwa mimi ninavyoona kwamba walionewa kwa sababu kwa mujibu wa kitabu cha...

SPIKA: Majibu ya maswali hayo Mheshimiwa Naibu Waziri.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Spika, bado swali langu.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri majibu.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Spika, swali langu la pili bado.

SPIKA: Tayari tayari tayari.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Spika, nakuomba, nimeulizaje?

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri majibu tafadhali.

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Spika, nimeulizaji?

SPIKA: Tayari tayari. (Kicheko)

MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Spika, hili la pili nimeulizaji? (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Selemani Said Bungara maarufu kama Bwege kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Bungara kwa pongezi alizozitoa kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi pale alipotoa ushuhuda wa namna ambavyo Serikali ya Chama cha Mapinduzi imefanya kazi kubwa ya usimamizi na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi katika kudhibiti uvuvi haramu wa kutumia mabomu, shukrani kwa kuwa muungwana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, Mheshimiwa Bungara analalamika kuwa kuna viongozi wa Serikali wanakatisha tamaa wananchi na akamtaja Diwani mahiri kabisa wa Kata ya Kivinje Mheshimiwa Jafar Arobaini na DAS wa Kilwa.

Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nijibu maswali haya kwa kusema kuwa nina mfahamu vyema Mheshimiwa Diwani Jafar Arobaini, ni mtu makini, na mtu mchapa kazi, mtu hodari, mzalendo, nina hakika kuwa hawezi kuwa kinyume na Serikali ya Chama cha Mapinduzi ambayo yeye ni Diwani wake. Kama itathibitishika ya kuwa wako viongozi wa BMU ambao wamefanya vitendo kinyume au yuko kiongozi yeyote wa Serikali aliyetenda kinyume sisi kama Wizara na Serikali kwa ujumla tuko tayari kwa hatua zetu za kinidhamu, kuchukua hatua na kufanyia kazi mambo haya.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili anasema juu ya nyavu zilizochomwa pale Kilwa, nyavu hazikuchomwa Kilwa peke yake; nyavu zimechomwa kote katika nchi maeneo ambayo yameonekana nyavu zile ziko kinyume cha sheria. Tumefanya hivyo katika eneo la bahari, tumefanya hivyo na tutaendela kufanya hivyo endapo tu watu watatumia nyavu zisizokuwa halali kwa ajili ya kulinda rasilimali za Taifa letu. (Makofi)
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Niseme kwa kweli kabisa kutoka katika upachupachu wa moyo kwamba mimi na mdogo wangu Mheshimiwa Mulugo hapa mbele yangu tumefurahishwa sana na majibu ya Serikali. Serikali imefanya utafiti, utafiti wa kisayansi na utafiti wa mwaka huu, Mheshimiwa Waziri hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo, nina maswali madogo mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa utafiti uliofanywa na Serikali unaonesha kwamba sababu zilizofanya samaki hawa wadumae ziko ndani ya uwezo wa Serikali, kwa mfano, uharibifu wa mazingira na uvuvi haramu, zote ziko ndani ya uwezo wa Serikali. Je, Serikali inafanya nini kuzuia huu uharibifu wa mazingira ili samaki warudi kama walivyokuwa zamani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri ni kijana mchapakazi sana na anatembea sana hapa Tanzania hajafika tu Chunya na Songwe, je, yuko tayari kufanya ziara Songwe ili mimi na Mheshimiwa Mulugo tuambatane naye kwenda kurekebisha kasoro hizi kwenye Ziwa Rukwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Senator, Mheshimiwa Victor Mwambalaswa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza uniruhusu kupokea shukrani kutoka kwa Mheshimiwa Mbunge Mulugo na Mwambalaswa kwa Serikali baada ya kutimiza ahadi ambayo imekuwa ikiombwa kila Bunge, kila msimu na Mheshimiwa Mulugo ya kwamba ni lini Serikali itafanya utafiti katika Ziwa Rukwa kujua sababu za udumavu na sasa Serikali ya Awamu ya Tano ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli imetekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza anauliza nini sisi Serikali tutafanya ili kuzuia uharibifu huu wa mazingira. Jambo hili ni mtambuka. Kama nilivyojibu katika swali la msingi kwamba sababu zinazosababisha kuharibika kwa mazingira zipo ambazo zinatokana na wachimbaji wadogo wadogo wa dhahabu wanaozunguka eneo lile ambao hawa kimsingi wanatumia teknolojia ya zamani ya kuchakata dhahabu kwa kutumia madini ya mercury kwa maana ya zebaki ambapo inatiririka na kuingia katika maji ya ziwa lakini vilevile nimezungumzia idadi ya mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa pamoja sisi katika Serikali, Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Madini na hata Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), tunao utangamano wa pamoja wa kuhakikisha kwamba hawa wachakataji wadogo wadogo wanaelimishwa na kuelekezwa namna iliyobora ya kuboresha uchimbaji na uchakataji wao. Naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mwambalaswa na jirani yake Mheshimiwa Mulugo kwamba hili tutalifanya kwa pamoja ikiwa ni pamoja na kutengeneza zile tunaita holding tanks kwa ajili ya maji yanayotoka katika uchakataji yaweze kuingia kwenye mifumo ile ya kudhibiti maji yale yasiende moja kwa moja katika maziwa yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili la kama niko tayari kufanya ziara. Nataka nimhakikishie kuwa tukimaliza hili Bunge niko tayari kabisa kwa ajili ya kwenda kufanya ziara kwenye eneo hili na kujionea mimi mwenyewe uharibifu wa mazingira na kuhamasisha Watanzania wanaofanya shughuli zile wafuate sheria na taratibu zetu. (Makofi)
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza katika jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli na mimi niipongeze Serikali, miaka yangu tisa ya kukaa hapa Bungeni nimekuwa nikiuliza swali la kufanya utafiti angalau Serikali sasa imeridhia na imefanya utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu moja la nyongeza, kwa kuwa Serikali imefanya utafiti na imeona kabisa kwamba kweli samaki wanadumaa kutokana na sababu walizozieleza lakini upo upande mwingine wa kuweza kupandikiza samaki wa aina nyingine katika Ziwa Rukwa kama ambayo mwaka 1978, Serikali ilichukua samaki kutoka Singida wakatuletea kule Ziwa Rukwa na tulikuwa tunawaita samaki aina ya Singida ambao ndiyo wameisha.

Je, Serikali iko tayari sasa kuangalia samaki wengine upande wa Ziwa Tanganyika, Nyasa au bwawa la Mtera hapa wakachukua wale samaki wakaja kuwapandikiza kwenye Ziwa Rukwa ili kuongeza idadi ya samaki katika ziwa hili?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Phillipo Mulugo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru kwa rai yako juu ya uwepo wa madini yale na umeelekeza Wizara ya Afya itakapokuja itaendelea kujibu jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie watafiti wetu wanatazama maana viko viwango ambavyo vimekuwa recommended na WHO ikiwa kama vitaonekana vimefikia au vimezidi basi zipo hatua ambazo sisi pamoja na Wizara ya Afya tutazichukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na jambo la Mheshimiwa Mulugo la namna ya kupandikiza samaki wengine kutoka maeneo mengine, naomba nichukue ushauri huu na tutakwenda kuufanyia kazi, ukionekana ni ushauri wenye kufaa basi tutautekeleza.
MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi ambazo Mheshimiwa Waziri amezieleza, kukosekana kwa miundombinu ya uogeshaji wa mifugo kumechangia katika kudumaza afya za mifugo na uboreshaji wa majosho nchini umekuwa kwa kasi ndogo sana:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa muda mfupi wa kuboresha majosho nchini katika maeneo ya wafugaji?

(b) Wizara ina mkakati gani wa kuhakikisha chanjo hizi muhimu zinapatikana kwa urahisi wakati wote?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2019/2020 jumla ya majosho 292 yamekarabatiwa nchini. Kati ya hayo, 161 yamekarabatiwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi na 131 yamekarabatiwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Majosho hayo yapo katika mikoa ya Singida, Iringa, Kagera, Katavi, Kigoma, Mara, Mwanza, Rukwa, Ruvuma, Shinyanga, Simiyu na Tabora.

Aidha, Wizara imetoa maelekezo kwa Halmashauri zote nchini kukarabati miundombinu ya mifugo yakiwemo majosho kwa kutumia fedha inayotokana na mapato ya ndani kutoka katika Sekta ya Mifugo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Wizara imetenga kiasi cha shilingi 100,000,000/= kwa ajili ya kukarabati majosho 125 katika Halmashauri za Wilaya 25 ikiwemo Singida.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea kuimarisha uzalishaji wa chanjo ndani ya nchi ambapo uzalishaji wa aina za chanjo katika Kiwanda cha Kuzalisha Chanjo za Mifugo (TVI) cha Kibaha umeongezeka kutoka chanjo aina nne mwaka 2018/2019 kufikia chanjo aina sita kwa mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Spika, aidha, jumla ya dozi 49,008,325 za chanjo zikiwemo dozi 47,347,700 za chanjo ya matone dhidi ya Ugonjwa wa Mdondo (TEMEVAC - I ), dozi 626,000 za Ugonjwa wa Kimeta, dozi 113,000 za Ugonjwa wa Chambavu, dozi 756,600 za Ugonjwa wa Mapafu ya Ng’ombe, dozi 19,275 za Ugonjwa wa Kutupa Mimba na dozi 145,750 za chanjo zenye muunganiko wa Kimeta na Chambavu (combination of Blackquarter vaccine and Anthrax vaccine - TECOBLAX) zimezalishwa na kusambazwa kwa wadau nchini.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeandaa utaratibu wa manunuzi ya chanjo kwa pamoja (Bulk Procurement) ambapo chanjo zote ambazo hazizalishwi hapa nchini zitaingizwa nchini ikiwemo chanjo za Magonjwa ya Mapele, Ngozi, Miguu na Midomo kwa pamoja na zitakuwa na bei elekezi na zitasimamiwa na Serikali ili kupunguza gharama ya chanjo kwa wafugaji.

Mheshimiwa Spika, aidha, kwa Mkoa wa Singida chanjo zinapatikana katika Kituo cha TVLA Kanda ya Kati kilichopo Dodoma.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa vile moja katika migogoro mikubwa ya wafugaji na wakulima yapo kwenye Kijiji cha Ngadinda, Halmashauri ya Madaba; na moja ya sababu ni kwamba wafugaji ambao wameambiwa wahame kwenye eneo la hekta 1,800 ambazo zilitolewa na Serikali kwa wakulima hawajahama. Nini kauli ya Serikali kuhusu kuwaondoa hawa wafugaji ambao wamekaa kwenye eneo ambalo lilitolewa kwa ajili ya kilimo? Ni lini wafugaji hawa wataondoka?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni lini Serikali sasa itachukua hatua za makusudi za kuwawezesha wafugaji nchini ili waweze kufanya ufugaji wa kisasa na hivyo kuondoa migogoro ya wafugaji na wakulima?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph Mhagama kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ukweli kwamba shamba la Serikali na Ngadida lililoko pale Songea lilikuwa na ekari 6,000 na miaka michache nyuma tuliligawa; 1,800 tukawapa wanakijiji na takribani 4,200 tukabaki nazo Serikali na kugawa vitalu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kusikia kauli ya Serikali. Naomba niseme kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tayari 1,800 tulishazigawa kwa wanakijiji kwa ajili ya shughuli zingine ikiwemo kilimo, sasa iwe ni marufuku kwa wale ambao hawakupewa eneo hilo kufanya shughuli nyingine za kuwaingilia wale wanaokwenda kufanya shughuli za kilimo kule. Na hili ninaielekeza halmashauri ya wilaya kulisimamia. Kinyume na hapo ndiyo linakwenda kusababisha migogoro isiyo ya lazima ya wafugaji kuweza kuingia katika maeneo ya wakulima.

Mheshimiwa Spika, mkakati wetu kwa jambo hili la pili la Serikali kuwawezesha wafugaji; hivi sasa tunaendelea na mkakati wetu wa kugawa vitalu katika maeneo yetu yote tunayoyamiliki; na vitalu hivi sasa tunakwenda kuviboresha. Tumetoa maelekezo kwa watendaji wetu kuongeza muda wa uwekezaji katika vitalu ili anayepewa kitalu aweze kuwa na muda wa kutosha na asiwe na wasiwasi juu ya uwekezaji wake.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo tumeielekeza Bodi ya Nyama kuhakikisha inatoa elimu ya kutosha juu ya unenepeshaji, na hivi sasa tunaunganisha na Benki yetu ya Kilimo iliyo tayari kuwapa mikopo watu wote waliojiweka katika utaratibu mzuri wa unenepeshaji. Na tayari tumeshatoa maelekezo kwa viwanda vinavyochakata nyama kutoa mikataba ya biashara kwa wanenepeshaji wote nchini ili waweze kutumia fursa hiyo ya kuweza kuongeza uchumi wa taifa letu vizuri.
MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali pia napongeza kazi inayofanywa na Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi na Halmashauri zake katika kutatua migogoro hii.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ni lini itajenga mabwawa kwa ajili ya kunywesha mifugo hiyo? Hapa tumeona katika jibu la msingi shida kubwa ni kugombania maji pamoja na malisho.

Mheshimiwa Spika, pili, tunaomba kazi hii ya kutatua migogoro katika Mkoa wa Lindi iharakishwe maana Sekretarieti ya Mkoa imeelemewa na migogoro hiyo. Je, Serikali inasemaje kuhusiana na suala hili?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tecla, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Lindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kwa kutambua umuhimu na katika mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan wa kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji, katika bajeti ya mwaka huu 2021/2022 tumetenga jumla ya shilingi milioni 900 kwa ajili ya kujenga mabwawa katika Mkoa wa Lindi. Bwawa moja litajengwa katika Wilaya ya Liwale na lingine katika Wilaya ya Nachingwea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, kwa kushirikiana na Serikali ya Mkoa wa Lindi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imejipanga vyema kwa kutumia Kamati inayoshughulikia migogoro ya ufugaji na wakulima kwenda kuweka kambi kuzungumza nao na kushirikiana katika kutafuta mbinu za kusuluhisha migogoro hii, ikiwa ni pamoja na kutatua lile tatizo la nyanda za malisho.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nasikitika kwa majibu ya Serikali, bado anarejea mwaka 1997 ilhali swali langu la msingi limerejea mwaka 2016 ambapo Waziri wa Mifugo by then alikuja na Watendaji wa Wizara, wakakaa na Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Mkoa Tarime, Rorya na Mkoa wa Mara na tukakubaliana kwa umoja wetu kwamba Mnada wa Kirumi Check Point uendelee na Mnada wa Magena uendelee kwa sababu uko mpakani ili ng’ombe zisipelekwe kuuzwa kwenye Mnada wa Maabel. Maswali yangu mawili ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kama Taifa tunahitaji mapato; na Waziri amekiri kwa mwaka 1996 tu Serikali ilipata maduhuli ya shilingi milioni 260 kwa kuuza ng’ombe 104,000; na huo Mnada wa Check Point tangu mwaka 2014 mpaka leo mmeuza ng’ombe 34,000 tu; ni dhahiri mnada wa mpakani una mapato zaidi: Je, ni lini sasa Serikali itarejea muhtasari wa Kikao ambacho tulifanya mwaka 2016 pamoja na kuambatana na Wizara husika ili twende kwenye Mamlaka ya Mkoa kuhakikisha kwamba Mnada wa Magena unafunguliwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; Mnada wa Kirumi hauchukui ng’ombe kutoka Serengeti, Rorya wala kutoka Tarime; ng’ombe zinatoka Tarime, Rorya na Serengeti zinaenda Kenya moja kwa moja; na sasa hivi hamna hayo mambo ya usalama, kuibiwa ng’ombe, hayapo kabisa Tarime; mkiendelea kuongea hivi ni kama mnadhihaki wananchi wa kule: Ni lini sasa mtahakikisha kwamba mnajiridhisha hamna wizi wa ng’ombe kutoka Tarime kwenda Kenya au kutoka Tarime kuja huko Kirumi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kwamba, tunakiri tunahitaji sana mapato na Serikali imejielekeza katika kuhakikisha kwamba mifugo na uvuvi inatoa mchango mkubwa katika pato la Taifa. Ni ukweli kwamba Mnada wa Magena uko mpakani na utoroshaji ni mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa rejea yako ya mwaka 2016 iliyofanywa ziara ya Mheshimiwa Waziri wa wakati huo
na viongozi wengine, Wizara ya Mifugo na Uvuvi tuko tayari kuhakikisha kwamba maoni haya uliyoyatoa Mheshimiwa Mbunge tunayachukua na kuendelea kuwasiliana na mamlaka za Mkoa na kufanya rejea na tathmini ili kusudi tuweze kwenda kwa pamoja na kuhakikisha tunaongeza wigo wa mapato sawa na matakwa na maelekezo ya Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa pale Pugu kwenye Jimbo la Ukonga kuna Mnada wa Upili na tulishafanya ziara pale na Naibu Waziri wa Mifugo na ziko ahadi alizitoa; tukiwa tunaelekea kwenye kipindi cha Bajeti, naomba kauli ya Serikali kuhusiana na maboresho ya mnada ule hasa miundombinu ya ukuta, njia za kuingilia na vitendea kazi vya watumishi. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kwamba Mnada wa Pugu ni mnada wa kimkakati na ni katika minada ambayo inaingiza fedha nyingi za maduhuli ya Serikali. Katika Bajeti ya Mwaka 2021/ 2022, Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi tumejipanga kuhakikisha kwamba Mnada wa Pugu unaboreshwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara kwa wakati huu tuko tayari kuhakikisha tunatumia mbinu za mapato yetu kuuboresha taratibu wakati tunaendelea kusubiri Bajeti Kuu ya mwaka 2021/2022.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika nashukuru, pamoja na jitihada kubwa na nzuri za Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, bado wavuvi wadogo hususan wa kutoka Mkoa wa Kagera, Geita, Mwanza, hawanufaiki ipasavyo hususan katika uuzwaji wa samaki aina ya sangara. Nasema hivi kwa sababu, mvuvi anapouza sangara kwenye viwanda vya kuchakata wanauza sangara pamoja na mabondo ambayo yanakuwa ndani ya sangara kwa Sh.4,500 mpaka Sh.8,000 kwa kilo. Mabondo haya yana wastani wa bei kidunia kati ya Sh.1,000,000 mpaka Sh.2,000,000 kwa kilo. Kwa hiyo ningependa kufahamu, je, ni lini Serikali itaweka kisheria kuhusiana na bei ya sangara na bei ya mabondo iwe tofauti ili wavuvi wadogo wa kutoka kata…

SPIKA: Mheshimiwa Neema K. Lugangira mabondo ni nini?

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, mabondo ni mfuko wa hewa ambao unakuwa ndani ya mdomo wa samaki unamsaidia samaki kuelea, lakini mabondo hayo yanatumika kama chakula kwa wenzetu kule wa Asia, lakini pia mabondo haya yanatumika kutengeneza vipuri vya ndege, yanatumika viwandani, inatengeneza mpaka nyuzi kwa ajili ya operesheni au mtu anapoumia. Zaidi ya hapo, mabondo hayo pia yanatumika kutengeneza plastiki mbalimbali, ndio maana yanakuwa na thamani kubwa sana.

Mheshimiwa spika, kwa hiyo kwa jinsi sheria ilivyo sasa hivi, mvuvi anapokwenda kuuza samaki aina ya sangara, anauza sangara pamoja na mabondo yake ndani kwa bei ya Sh.4,500 mpaka Sh.8,000. Wakati haya mabondo peke yake yanaingizia Serikali kiwango kikubwa cha fedha kwa sababu bei ya kidunia kilo moja ya mabondo ni kati ya sh.1,000,000 mpaka Sh.2,000,000. Sasa je, Serikali ina mpango gani wa kuangalia suala hili kisheria ili yule sangara anapouzwa bei iwe tofauti kwa sangara na bei iwe tofauti kwa mabondo?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, ni kwamba katika sekta ya uvuvi lipo kundi maalum la wanawake. Wanawake wana mchango mkubwa sana katika kukuza uchumi wa Taifa letu, lakini bado kumekuwa na changamoto kubwa ya vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake wanaojihusisha na sekta hii ya uvuvi. Wengi wao tukiwaliuza wanasema changamoto hii inatokana na kwamba wanawake hawana mitaji ya kutosha ya kuendesha kambi. Kule kwenye kambi wanakuwepo wanawake wanajihusisha na shughuli za uvuvi, lakini kuna ukatili wa kijinsia mkubwa sana unaoendelea.

Mheshimiwa Spika, sasa ningependa kuiuliza Serikali, je haioni iko haja ya kutenga angalau asilimia 20 kutoka Mfuko wa Kuendeleza Uvuvi Nchini kwa ajili ya wanawake wanaojihusisha katika zao la samaki? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Lugangira, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mabondo ni kweli, ni boya, lililoko tumboni mwa samaki linalo msaidia katika zoezi zima la kuelea. Kwa miaka ya hivi karibuni biashara ya mabondo imekuwa ni biashara mpya, ambayo imeonekana kuwa na soko kubwa katika Nchi za Asia. Sheria na Kanuni tulizonazo hivi sasa, mabondo ni zao linalotokana baada ya kuchakatwa samaki. Kwa hiyo, kiwanda ambacho kinachakata samaki anapelekwa samaki akiwa mzima mzima.

Mheshimiwa Spika, kwa Mujibu wa Sheria za Usalama wa Chakula na Ubora wake, ni lazima yule samaki anavyofikishwa pale kiwandani apelekwe akiwa mzima mzima katika umbile lake lote. Kwa hiyo, baada ya kumchakata, ndio sasa yanapatikana mabondo na mazao mengine ambayo yote sisi katika Sheria ya Uvuvi tunayatambua ikiwemo ile skeleton, lakini vilevile kichwa, mikia, ngozi na hata mafuta ya samaki yanayopatikana katika mwili wake.

Mheshimiwa Spika, mabondo yanachukua kati ya asilimia 1.8 mpaka asilimia 2.0 ya uzito mzima wa yule Samaki. Kwa hiyo, ili upate kilo moja ya mabondo inakuhusu uwe na samaki zaidi ya mmoja, watatu, wanne hadi watano, ndio utapata kilo moja ya mabondo. Yenyewe ukubwa wake yanatokana na ukubwa wa yule samaki mwenyewe. Hata hivyo, niseme tu kwamba, rai na ushauri wa Mheshimiwa Neema Lugangira ni mzuri. Kwa kuwa sasa tupo katika utaratibu wa kuboresha sheria yetu, jambo hili ni jema, tunalichukua na sisi Serikalini tutakwenda kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, amezungumzia juu ya wanawake wachakataji na wafanyabiashara ya samaki na ukatili wanaofanyiwa katika shughuli zao hizo.

Kwanza, Sheria yetu ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003, Kipengele cha 29 kinakubali na kinatoa mamlaka kwa Wizara kuunda Mfuko wa Kusaidia Uvuvi, kwa maana hiyo pia, vilevile, sera yetu ya Uvuvi ya mwaka 2015, tumeiboresha na katika kuboresha kwetu tumeweka jambo maalum la kuwasaidia wanawake na kwa hiyo, tutakuwa na jukwaa la kusaidia wanawake. Vilevile kama hiyo haitoshi, tutatambua moja kwa moja wanawake hawa wachakataji wa samaki.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimpongeze vilevile Mheshimiwa Neema Lugangira kwa kuwa akinamama hawa wanaoshughulika na shughuli za uvuvi na uchakati na wafanyabiashara wa samaki ni miongoni mwa wapiga kura waliopiga kura kuhakikisha kwamba yeye na Wabunge wengine akinamama wanaingia humu Bungeni na kwa hivyo amechukua jukumu la kutukumbusha kama Serikali na tutalifanyia kazi ipasavyo. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mifugo, naomba nipate nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, sekta ya nguruwe sasa imekuwa ikikuwa kwa kasi kubwa sana na hapa nchini na kwamba ufugaji wa nguruwe ni rahisi kidogo kuliko mifugo mingine kwa sababu wanatunzwa ndani ukilinganishwa na ng’ombe, sasa kumekuwa na incentives mbalimbali zinazotolewa kwenye mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye bidhaa zinazosaidia kwenye ufugaji wa nyuki, samaki, kuku ng’ombe na mifugo mingine zina nafuu ya kodi. Je, kwa sababu sekta hii nayo inahitaji kuboreshwa na kuwa ya kisasa zaidi Serikali haioni kuna haja ya kutoa incentives kwenye vifaa vinavyotumika kwenye ufugaji wa nguruwe kwenye eneo la kodi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kumekuwa na muingiliano mkubwa sana kwenye sekta ya nyama, huko utakutana na watu wa NEMC utakutana na watu wa TBS, ambao wanashughulika machinjio wengine usafirishaji, na wengine ubora wa nyama kitu ambacho kinasababisha mazao ya nyama kuwa na gharama kubwa sana ambayo Watanzania wengi hawawezi ku-afford kununua na kilo bei ya nyama ukiangalia katika mchanganuo wake gharama ya uununuzi inatokana mwingiliano huu wa mamlaka mbalimbali zinazosimamia suala la nyama sasa swali langu.

Sasa swali langu, Serikali haioni haja ya kuhamisha shughuli zote zinazofanywa na idara mbalimbali ili zikasimamiwe na Wizara na Mifugo ambayo yenyewe ndio yenye uwezo mkubwa sana wa kusimamia kutokana na utaalamu uliopo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa
Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Ndanda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ni juu ya incentives kwa ajili ya wafugaji wa nguruwe kama ambavyo wanapata wafugaji wengine. Naomba niichukue rai hii ya Mheshimiwa Mwambe ya kwamba Serikali tuitazame ufugaji wa nguruwe na kwa kuwa tuo kwenye kipindi cha bajeti jambo hili limekuja kwa wakati muafaka na Serikali tunalichukua, litatazamwa katika vikao vyetu kadri itakavyoonekana inafaa, wataalam pamoja nasi viongozi tutashauriana kwa ajili ya kuhakikisha kwamba ukuaji wa tasnia hii ya nguruwe inakwenda sambasamba na ukuaji wa mifugo mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ameuliza juu ya suala zima la muingiliano mkubwa wa taasisi mbalimbali za Serikali unaopelekea kupandisha bei ya nyama na mazao yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika awamu iliyopita Serikali ilifanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha kwamba tunaunganisha vyombo vyetu vinavyosimamia tasnia zetu hizi, kwa mfano baadhi ya mazao yatazamwe na moja tu katika taasisi, miaka michache iliyopita tuliamua kwa dhati kabisa kwamba TMDA itatazama vyakula na kwa upande wa mazao ya mifugo yatatazamwa na wataalam wenyewe wa mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikuhakikishie ya kwamba rai yako yakuondoa mgongano huu wa kitaasisi na la lenyewe tumelichukua kwa kusudio la kupunguza changamoto inayowapata wafanyabiashara wa mazao ya mifugo na wafugaji pia vilevile. (Makofi)
MHE. SEIF K. GULAMALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kuwepo na milipuko ya magonjwa kwenye mifugo, nini mpango wa Serikali wa kujenga majosho katika Wilaya ambazo zina mifugo mingi hususani Wilaya ya Igunga kutuwekea majosho kwenye minada na vijiji? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Seif Gulamani, Mbunge wa Manonga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejipanga vyema katika kuhakikisha kwamba tunajenga majosho ya kutosha katika vijiji na Wilaya mbalimbali nchini. Katika mwaka huu tunaokwenda nao wa 2020/2021 Wilaya ya Igunga kwa maana ya Jimbo la Manonga ni miongoni mwa maeneo yatakayopata fursa ya kujengewa majosho, tena utapata pale majosho mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile habari njema kwa Waheshimiwa Wabunge wote; mkakati wa Serikali katika muda wa miaka hii mitano, baada ya kuwa tumefanikiwa sana katika zoezi letu la uogeshaji wa mifugo na kupunguza sana magonjwa yanayoambukizwa kupitia kupe, tutaendelea na zoezi hili la uogeshaji na kwa kujenga majosho ya kutosha. Tunataka kila kijiji ambacho kina wafugaji kipate josho na kwa hiyo tunaomba sana mtuunge mkono katika kuhakikisha kwamba zoezi hili linafanikiwa. (Makofi)
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, jitihada ambayo inatumika na Wizara hii katika kukamata wale wanaotumia nyavu ambazo hazifai au katika masuala mengine yanayohusu kukusanya mapato ni kubwa sana kuliko zinazotumika katika kuwawezesha hawa wavuvi na ndiyo maana kuna wakati nilisema kwa nini wavuvi wameendelea kuwa maskini kuliko sekta nyingine. Nauliza swali hili kwa sababu Wizara yenyewe iliamua kutoa ruzuku ya injini za boti, lakini kwa kuwafanya hawa wananchi lazima wakae kwenye kikundi ni sawa na kuwafunga miguu yule mwenye ari ya kufanya kazi akimbie anamsubiri mwenzake ambaye anatakiwa mpaka achangie. Je, ni lini Serikali itaangalia upya suala hili ili kuwawezesha wavuvi hawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Ziwa Nyasa lina mawimbi makubwa sana kiasi kwamba kuvulia ile mitumbwi midogo midogo ambayo haina injini inakuwa ni changamoto kubwa kwa hawa wavuvi, kiasi kwamba sasa inafikia mtu mwenye injini moja ya boti inabidi avute mitumbwi mitatu mpaka minne kwenda kilindini na kurudi, jambo ambalo ni hatari na wale wanaoenda kuvua wanazama kila wakati hata juzi kuna mvuvi amepotea. Je, Serikali ina mpango gani wa kuimarisha, kuwezesha na kutoa mafunzo kamilifu kwa wavuvi hawa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Engineer Stella Martin Manyanya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza uniruhusu nimpongeze sana Mheshimiwa Stella Manyanya kwa namna ambavyo amekuwa mstari wa mbele kuwapigania jamii ya wavuvi wa Ziwa Nyasa. Naomba nimhakikishie kwamba Serikali imejipanga vyema katika kuhakikisha wavuvi wote nchi wanapata suluhu ya changamoto zinazowakabili wakiwemo wavuvi wa Ziwa Nyasa na ndiyo maana katika wakati huu tulionao Serikali imejipanga kwenda kuhakikisha tunajenga soko la kisasa katika eneo la Mwambao wa Ziwa Nyasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lini Serikali itaangalia upya suala la kuwezesha wavuvi mmoja mmoja. Sera yetu ya Vyama vya Ushirika ukiitazama vyema na lengo letu ni katika kuhakikisha kwamba wavuvi hawa wanakuwa na sauti ya pamoja. Ni kweli tunaweza tukawasaidia na tuko katika kuwasaidia kuhakikisha kila mmoja mwenye nia njema aweze kufikia lengo la kuwa na mashine na ikiwezekana awaajiri na wenziwe. Hata hivyo, wanapokuwa pamoja ni kwa ajili ya kuwawezesha kuwa na sauti ya pamoja kulifikia soko, ili kuwarahisishia kutokubanwa na kulaliwa na wateja.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Waheshimiwa Wabunge tuliunge mkono jambo hili na sisi Serikali tumekubaliana kuhakikisha tunaongeza jitihada kwenye kupeleka mikopo kama vile ya VICOBA, mikopo kupitia Benki ya Kilimo na madirisha mbalimbali ya benki za kibiashara ili yaweze kuwasaidia hata mvuvi mmoja mmoja ambaye atakwenda kuajiri wavuvi walio wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya suala la kutoa elimu; utoaji wa elimu ni jambo endelevu. Nimpe pole sana Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya kwa ajali zinazowapata wavuvi katika eneo la Ziwa Nyasa na maeneo mengine ya wavuvi wote na sisi tumejipanga sana kupitia Chuo chetu cha FETA cha Utaalam wa Uvuvi kuhakikisha tunapeleka elimu ya kutosha katika maeneo yote ya wavuvi ili waweze kushindana na kuhakikisha kwamba wanakuwa tayari kuendana na hali halisi hasa za kimazingira na ili kuondoa uwezekano kupatikana kwa hizi ajali ambazo zinawapata wavuvi wa kule Nyasa.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na vyama vya ushirika walivonavyo wavuvi lakini bado wavuvi wetu wana hali duni sana kiuchumi katika ukanda wetu wa Pwani. Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuwakwamua wavuvi wa pembezoni mwa Bahari ya Hindi kwa Mikoa ya Tanga, Dar es Salaam, Pwani, Lindi na Mtwara katika kushiriki kwenye uchumi wa blue.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Zodo; kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan inao mkakati madhubuti au inayo mikakati madhubuti ya kuhakikisha inawasaidia wavuvi wa ukanda wa Pwani hasa kuendana na uchumi wa blue kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti tunayoitarajia ya mwaka 2021/2022, yako mambo ya msingi yatakayofanywa. La kwanza ni kuhakikisha tunaongeza uzalishaji katika miamba ya kuvutia Samaki, tutatengeneza katika Ukanda wote wa Pwani. Vile vile kama haitoshi tutahakikisha kwamba tunatengeneza vichanja vya kukaushia samaki, sababu moja kubwa inayowasumbua wavuvi ni upotevu wa mazao ambao wanayazalisha kwa kuoza na kwa kuharibika. Tunataka tuhakikishe kwamba samaki wote wanaozalishwa na wavuvi wa ukanda wa pwani hawaharibiki kwa sababu tutawaongezea thamani kwa kuwakausha, lakini vile vile tutakwenda kuongeza uzalishaji wa barafu na kuwa na cold rooms za kutosha katika ukanda mzima wa pwani, ili kuweza kuitumia vyema uchumi wa blue na kuongeza kipato cha mvuvi mmoja mmoja na hatimaye kuongeza kipato cha Serikali yetu. Naomba wavuvi watuunge mkono ili kuweza kufikia lengo hilo.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa maelezo yake mazuri kwenye swali langu la msingi. Sasa ningeomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Serikali ina mkakati wa kukuza uchumi wa bluu, je, Wizara yake ina mpango gani wa kutoa elimu ya teknolojia kwa wavuvi wa Bara na Visiwani ili kukuza uchumi wao na pato la Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa kuwa Serikali tayari imeagiza meli nane, nne Bara na nne Zanzibar. Je, Serikali au Wizara ina mpango gani wa kutoa elimu kwa maofisa hao watakaohudumia meli hizo pamoja na ajira kwa vijana ambao ajira sasa hivi ni ngumu na meli hizo zitasaidia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, msimamo na mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ni juu ya kutumia vyema fursa ya uchumi wa bluu. Katika kutekeleza jambo hilo Serikali ya Awamu ya Sita imejipanga vyema kuhakikisha kwamba teknolojia ndiyo itakayotuongoza ili tuweze kutumia vyema rasilimali zilizopo katika bahari yetu lakini vilevile na maziwa makuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, teknolojia hii ni pamoja na kuwasidia wavuvi waweze kutumia vifaa vya kisasa vitakavyowafikisha katika maeneo yenye samaki kwa urahisi na kwa kutumia gharama nafuu. Vifaa hivi, hivi sasa Wizara ipo katika mkakati wa kuhakikisha kwamba tunajipanga vyema watumie GPS, mvuvi anapotoka pwani anapokwenda baharini, awe tayari anazo taarifa za wapi samaki wanapatikana ili hiyo iweze kumsaidia kuweza kufanya timing ya muda, lakini vile vile hata mafuta atakayoyatumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili analotaka kujua ni juu ya mkakati wa Serikali kwenye kuutumia uchumi huu wa bluu kutoa elimu na ajira kwa vijana na akinamama. Serikali zote mbili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kutambua umuhimu wa uchumi wa bluu, meli nane kama alivyotaja zitanunuliwa nne kwa upande wa Zanzibar na nne kwa upande wa Tanzania Bara. Kwa kufanya hivyo Mashirika yetu makubwa mawili ya ZAFICO na TAFICO yanafufuliwa na yatanunua meli mbili kwa kuanzia katika mwaka wa fedha huu 2021/2022. ZAFICO kwa maana ya Zanzibar Fisheries Corporation itanunua meli mbili na TAFICO itanunua meli mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa zitapatikana ajira kwa vijana wa Kitanzania ambao pia watapewa elimu ya kuweza kujiandaa na fursa hiyo kubwa. Zaidi ya hapo tunao mpango wa maendeleo ya kilimo kwa maana Agricultural Sector Development Program II itakwenda sambamba na kutengeneza na kuwaandaa vijana wetu ikiwa ni pamoja na shughuli nzima za ufugaji wa samaki katika maeneo ya bahari, tunaita kwa lugha la kitaalam Mariculture. Zaidi ya vijana 1,000 kule Zanzibar na akinamama zaidi ya 15,000 watanufaika na mradi huu wa AFDP. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge waendelee kutuunga mkono na wananchi wajipange vyema kuhakikisha tunatumia fursa hii ya uchumi wa bluu. Ahsante sana.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwanza nimpongeze kwasababu Mheshimiwa Naibu Waziri ni mtaalam sana katika mambo ya uvuvi na ni imani yangu kwamba majibu yake yamesikilizwa kwa makini na watu wa Mkuranga pamoja na Kibiti. Maswali yangu mawili ya nyongeza ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kibiti hasa katika maeneo ya Delta kuna kata kama tano kuna Kata ya Kihongoroni, Kata ya Mbochi, Kata ya Maparoni, Kata ya Msara na Kata ya Salale vile ni visiwa shughuli zao kubwa wanazozitegemea ni uvuvi wa hawa Kambamiti hatuna shughuli nyingine yeyote ya kilimo. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka umefika kuweza kutoa Muarobaini wa tatizo hili la muda wa uvuvi kwamba wananchi hawa waruhusiwe kuanzia kipindi cha mwezi wa 12 mpaka mwezi wa tano? hilo ni swali la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili tunajua Kambamiti wanapatikana Kibiti na sisi kama watu wa Kibiti tunapenda sana kuona rasilimali ile inawanufaisha vile vile Watanzania wengine yaani kuchangia pato la Taifa. Je, Serikali ina mkakati gani ili sasa kuweza kuhakikisha Kambamiti wale wanawanufaisha sio tu wananchi wa Kibiti Halmashauri lakini vile vile kuongeza pato la Taifa? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la ndugu yangu Mheshmiwa Mbunge wa Kibiti Comrade Twaha Mpembenwe. Kwanza naomba nikiri swali hili ni la muhimu sana kwa wananchi wa Wilaya ya Kibiti na wale wa Jimbo langu la Mkuranga, anataka kujua ni mbinu na mkakati gani muarobaini tutakaokuwa nao wa kuhakikisha kwamba wanachi hawa wa maeneo ya kisiju maeneo ya Mdimni, maeneo ya Nganje, maeneo ya Kifumangao, maeneo ya Nyamisati, maeneo ya Mfisini, maeneo ya Kiasi, Mbwera mpaka kule mpakani na Kilwa kwa maana ya Marendego.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa maana Wizara imejipanga vyema tumeshaelekeza mahsusi kabisa kwamba Shirika letu la utafiti la TAFIRI kwa kushirikiana na idara yetu kuu ya uvuvi ifanye mapitio ya utafiti tuliokwisha kuufanya na sasa tutakwenda kufanya zaidi kwa kushirikiana na wananchi wenyewe na wadau katika maeneo yote haya ili tupate suluhu ya kudumu ni ukweli usio pingika, kwamba wananchi wa maeneo haya wao wamekuwa wakihifadhi maeneo haya Samaki wanapokuwa wamekuwa wanaondoka Bahari kuu na sasa matokeo yake hawana uwezo wavuvi wale wa kuwafikia Samaki wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeelekeza pamoja nami Mheshimiwa Waziri kwamba tufanya kazi ya kutoka nje kuondokana na yale mazoea ya kuwazuia tutafuta alternative ambayo itawafanya wananchi hawa sasa wawe na uwezo wa kuweza ku-enjoy rasilimali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ametaka kujua juu ya mkakati wetu, ni namna gani tutawasaidia. Wananchi hawa hawana jambo jingine la kufanya hakuna kilimo kinachoenea kikakubali katika eneo lile isipokuwa uvuvi tu wa Prawns kwa maana ya Kambamiti, ni maelekezo tuliyoyatoa pia tutafute njia mbadala za kuwasaidia waweze kufanya uzalishaji zaidi katika miaka mitano iliyopita wananchi wa Mkuranga na Kibiti wamezalisha tani 1,200 zenye thamani ya shilingi bilioni 16 na zikaingiza Serikalini Milioni 600 sasa tunataka tutoke hapo tuongeze uzalishaji zaidi ili na wao waweze kuondokana na umaskini ambao ulioenea katika eneo hili wakati wamekalia rasilimali kubwa sana. Nashukuru sana.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna tatizo soko la Feri Dar es Salaam, wavuvi wanashindwa kusajili vyombo vyao mpaka wazungumze chini ya meza na hasa Zone Na.8, hebu itolee maelezo. (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana Mheshimiwa Mussa Azan Zungu, Mbunge wa Ilala ambapo eneo la Feri linamiliki wapiga kura wake. Kwa mujibu wa Sheria yetu ya Uvuvi ya mwaka 2003 Na. 22 haitambui mtoaji wa leseni kuwa mtu mwingine yeyote isipokuwa Mkurugenzi wa Halmashauri kupitia Idara yake ya Uvuvi ama Afisa mwingine yeyote aliyeidhinishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa kama Feri soko ambalo linamilikiwa na Manispaa ya Ilala kuna vitendo visivyokuwa vya vya uvunjifu wa sheria, kama ulivyosema watu wanatoa rushwa, natoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala na mamlaka zote pale Ilala zishughulike na jambo hili. Hawa wanaofanya vitendo hivi tumepata taarifa za awali na vyombo vyetu vya dola vinafanyia kazi kwamba wako viongozi wa sehemu inayoitwa Zone Na.8 wanafanya vitendo visivyo vya kiungwana vya kuwa-force wavuvi kutoa rushwa ndiyo wasajiliwe, hiyo ni kinyume cha sheria. Kwa hiyo, vyombo vyetu vitachukua hatua stahiki na jambo hilo liachwe mara moja.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuongeza nguvu kwenye uchumi wa bahari, Serikali wakati ikijibu swali la Mheshimiwa Mama Salma Kikwete, Mbunge wa Mchinga katika Bunge lililopita iliahidi kuwasaidia wavuvi wa ukanda wa bahari ya Mkoa wa Lindi vifaa vya uvuvi na hasa boti ya kusaidia uvuvi wao.

Kwa kuwa ahadi hiyo imechukua muda mrefu na muda unakwenda, wakati Serikali ikijipanga kuitimiza ahadi hii, je, iko tayari kuwasaidia walau mashine ndogo ndogo ziwasaidie kuboresha uvuvi wao wavuvi wa eneo hili hasa wanaotoka Jimbo la Mtama?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nape Moses Nnauye, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuko tayari, tutapeleka mashine kwa wavuvi wa Mchinga na Mtama. Nataka tu nimhakikishie kwamba tunao mpango mkubwa zaidi wa kuwawezesha wavuvi wa Ukanda wa Pwani In Shaa Allah katika bajeti yetu hii ya 2021/2022 mambo yatakuwa mazuri sana katika kuhakikisha kwamba wanafanya vizuri katika shughuli zao za uvuvi.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza naishukuru Serikali kwa majibu mazuri, lakini nilikuwa naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. La kwanza, kwenye shamba hili Serikali imeeleza kwamba inaweza ikatenga shilingi bilioni sita kwa maana ya mwaka 2021/2023.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nauliza: Je, Serikali iko tayari kuingia partnership kwa sababu Benki ya TADB (Tanzania Agriculture Development Bank), iko tayari kutoa hizi fedha na ikafanya iwekezaji kwenye shamba hilo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni maslahi ya wafanyakazi wa shamba lile kwa maana ya vifaa na madeni ya wafanyakazi wale, kwa muda mrefu hawajalipwa: Je, ni lini Serikali itakuwa tayari kuhakikisha maslahi ya wafanyakazi na pia vifaa vya shamba viwe vinanunuliwa?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, juu ya uwekezaji, tuko tayari na milango yetu iko wazi, karibu sana tuweze kujadili jambo hilo. Jambo la kuboresha maslahi ya wafanyakazi na ununuzi wa vifaa ni sehemu ya pesa zilizopangwa kutumika katika bajeti hii. Kwa hiyo, tunalielekea pia.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na maswali mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, tatizo lilolopo Chalinze ni sawa na tatizo lililopo Bagamoyo na hasa katika Vijiji vya Mkenge Kidomole pamoja na Vijiji vya Milo. Sasa swali langu ni kwamba, kutokana na tatizo la wakulima na wafugaji eneo lililotengwa halitoshi, ni dogo sana kwa vijiji hivyo. Ni lini Serikali itaongeza hili eneo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, Serikali inazingatia sana maoni na ndiyo maana hata maoni uliyoyatoa ni katika sehemu ya mpango wetu wa bajeti tunayokwenda ya kuboresha zaidi NARCO ili iweze kukidhi haja ya kuhakikisha kwamba wadau wetu mnafurahi na kuweza kutumia fursa ya ardhi hii kubwa na nzuri ya Serikali kuweza kufanya shughuli za uzalishaji kupitia mifugo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa hili la Bagamoyo Serikali iko tayari kupokea tena maombi ya wananchi na kuyafanyia kazi kwa ajili ya kuweza kuondoa kabisa migogoro ya wakulima na wafugaji.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu yasiyoridhisha ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Mheshimiwa Naibu Waziri ana mpango gani wa kuhakikisha kwamba, malalamiko haya ambayo yamedumu kwa kipindi kirefu sasa yanafikia mwisho?

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili, je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza akaji-committ ni lini atakutana na wadau wa biashara ya dagaa wanaosafirisha kutoka Zanzibar kwenda Tunduma, ili kuhakikisha kwamba, anazungumza nao kuhusu hizi kadhia na kuzimaliza? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, lini yatafika mwisho malalamiko haya ya wafanyabiashara wa dagaa. Nataka nimhakikishie kwamba, tumeweka utaratibu mzuri wa kufunga lakiri. Dagaa wanaotoka Zanzibar kupita katika Bandari ya Dar –es - Salaam wanapita katika utaratibu wa magunia yaliyo wazi. Tumeweka utaratibu ndani ya Serikali kwamba, wanapifika katika Bandari ya Dar - es - Salaam ni lazima tuyafunge lakiri ili kuthibitisha kama huu mzigo tayari ulishalipiwa ushuru kwa upande wa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, nakiri yawezekana wako watumishi, baadhi, wasio waaminifu wanaoleta vitendo visivyokuwa vya kiungwana. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wafanyabiashara wote, tutashughulikia jambo hilo hatua kwa hatua na vyombo vyetu vya dola vitakuwa vikifuatilia ili hao watumishi watakaokuwa wanabainika kufanya vitendo visivyokuwa vya kinidhamu tuwachukulie hatua na kuwarahisishia wafanyabiashara wetu kazi yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu lini nitakwenda kukutana na wadau wetu. Nataka nimhakikishie kwamba, mara baada ya Bunge la Bajeti, ikimpendeza yeye na Wabunge wengine wanaoguswa na jambo hili niko tayari kuandaa mkutano huo kwa ajili ya kukamilisha zoezi hili. Ahsante.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Ziwa Nyasa lina Kata zisizopungua nane; Kata ya Ruhuhu, Manda, Iwela, Lupingu, Lifuma, Makonde, Kilondo na Ruhila. Je, ni lini Serikali inakusudia kupeleka vifaa vya uvuvi kama engine za maboti kwa vikundi vya wavuvi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningetamani kufahamu ni lini Serikali itapeleka kituo cha kufanya utafiti wa samaki na viumbe maji huko Wilayani Ludewa maana kata hizi zina wakazi wasiopungua 28,000 ambao wanatumia ziwa hili kama swimming pool na njia tu ya usafiri. Ningependa kufahamu commitment ya Serikali juu ya kupeleka kituo cha utafiti wa samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kamonga, Mbunge wa Ludewa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, juu ya kupatikana kwa vifaa vya uvuvi katika makundi ya vijana kwenye Kata za Ruhuhu, Manda, Makonde na kwingineko katika Jimbo lake la Ludewa naomba nimhakikishie kwamba katika mwaka wa fedha huu ambao leo tunaendelea kujadili bajeti yake, Serikali imejipanga kuhakikisha vijana wote waliopo katika maeneo hayo na wenyewe wanaweza kuwezeshwa kupata vifaa vya kufanyia shughuli zao za uvuvi.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kituo cha utafiti; Ziwa Nyasa ni katika maeneo ambayo Shirika letu la Utafiti la Uvuvi (TAFIRI) litakwenda kufanya utafiti kule na uwezekano wa kuweza kupata kituo kidogo pale kwa ajili ya utafiti kwenye eneo la Ziwa Nyasa upo na naomba nichukue jambo hili nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itafanya jitihada ya kuhakikisha kituo kinapatikana pale ili na Ziwa Nyasa wakati wote liwe linatazamwa na kuangaliwa kwa karibu. (Makofi)
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; bado wavuvi wanalazimika kwenda mbali kwa ajili ya kutafuta samaki kutokana na changamoto mbalimbali za bahari na uhifadhi wa mazalia ya samaki, jambo ambalo linasababisha pia wavuvi hao muda mwingine wanapata ajali za baharini, wanapotea wenyewe pamoja na vyombo vyao.

Je, Serikali ina mkakati gani wa utoaji wa mafunzo kwa wavuvi hasa mafunzo ya uhifadhi wa mazalia ya samaki na hasa kwa wavuvi ambao wanatokea pande za Nungwi, Matemwe na sehemu zingine ambao wanatokea katika ukanda wa Zanzibar? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asya Mwadini Mohammed, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka huu wa 2021/2022 kwenye mpango wetu tumeweka mkakati maalum, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa pamoja tunao mpango madhubuti kwa kutumia mashirika yetu ya Deep Sea Fishing Authority (Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu), lakini vilevile kwa upande wa Tanzania Bara (TAFIRI) na kwa upande wa Zanzibar (ZAFIRI) tumeshafanya partial marine monitoring program ambayo tumeainisha maeneo yetu ya mavuvi.

Mheshimiwa Spika, lengo letu tunataka tuwatoe wavuvi wetu kwenye kufanya uwindaji, sasa tunakwenda katika uvuvi wa kidigitali. Mvuvi kabla hajakwenda kuvua, kupitia vituo vyetu aidha Ofisi za Vijiji au MBU au kwingineko apate taarifa za mavuvi, wapi walipo samaki, umbali anaokwenda; kwa hiyo, tutakuwa na mfumo wa GPS utakaokuwa ukiwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaamini kwamba mfumo huu utawawezesha wavuvi wetu watumie gharama ndogo sana ya mafuta, lakini vilevile wasitumie muda mwingi wa kwenda kuwinda. Tunataka tutoke katika uvuvi wa kuwinda twende katika uvuvi wa uhakika zaidi, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza kwa kuwa, karibu wenyeji wote wa Jimbo la Kawe wanajishughulisha na shughuli za uvuvi mdogo mdogo hasa wa mitumbwi na mara nyingi hutokea ajali hasa wakati wa usiku na kuhatarisha wavuvi wetu. Ni lini sasa Serikali italeta Boti angalau Fiber Boat ndogo ndogo, kwa ajili ya kuokoa panapotokea madhila ya namna hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Kata ya Msasani, Kata ya Kawe, Kata ya Kunduchi, Kata ya Mbweni, Mbezi pamoja na Bunju yote hiyo ni wavuvi wadogo wadogo wanaotumia mitumbwi na mikopo ya halmashauri haiwapi nafasi kwa sababu ina ukomo wa miaka 35. Ni lini sasa Serikali itakuwa na mpango maalum wa kuwapa mikopo hawa wavuvi ili kusudi kuboresha uvuvi wao?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ni kuhusu usalama wa wavuvi na uokozi pale wanapopata madhila mbalimbali baharini. Serikali kwa pamoja Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kupitia Police Marine lakini na Wizara ya Ofisi ya Waziri Mkuu zote zinafanya kazi kwa pamoja na hivi sasa ninavyozungumza, tuko katika mkakati wa kuhakikisha kwamba, panapatikana chombo au vyombo ambavyo vitakuwa vikifanya kazi hiyo ya doria na jambo hili linaratibiwa vyema na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa hivyo, wananchi wa Kawe na wenyewe wamo katika mpango wa namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, Jambo la pili ni kuhusu mikopo. Mheshimiwa Askofu Gwajima, Mbunge wa Kawe nataka nikuhakikishie kwamba, tumejipanga vyema na katika bajeti yetu ya awamu hii ya 2021/2022 Serikali ya Awamu ya Sita ya mama Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan imejipanga vyema nataka nikukaribishe kwa ajili ya kuhakikisha vikundi na vijana wa pale Kawe waweze kupata mashine za boti lakini vilevile waweze kujiunga katika vikundi vitakavyowasaidia kutengeneza vichanja vya ukaushaji wa samaki na hata kutengeneza mashine za kuzalisha barafu wauziane wao wenyewe kwa ajili ya kuondosha tatizo la upotevu wa mazao. Ahsante.
MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa majibu mazuri ya Wizara lakini nilikuwa na maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa Serikali imerahisisha upatikanaji wa vifaa, lakini pia tumeona vijana wengi wamejitokeza na wamehamasika kuingia katika sekta ya uvuvi na wengi wameunda vikundi, lakini hawajapatiwa mafunzo, lakini pia hawana vifaa vya kisasa vya kuvulia.

Je, ni lini kauli ya Serikali kwa vijana ambao wamejiunga kwenye vikundi na wamekidhi vigezo lakini awajapatiwa vifaa vya kuvulia na mikopo?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili tunaona kabisa kwenye majibu ya msingi ya Mheshimiwa Naibu Waziri anasema kwamba mahitaji ya wavuvi wa Tanzania na yaliyopitishwa ikiwa ni 2.6 bilion lakini hela iliyotolewa ni milioni 500 plus ambayo hii ni chini ya asilimia 25.

Je, ni nini mpango wa Serikali katika kuhakikisha tunaongeza kipato hiki hili wavuvi wakaweze kupata tija na uvuvi uweze kuwa na tija kwa nchi hii kwa kuongeza ajira kwa vijana na kipato cha Taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sylivia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, uniruhusu pia nimpongeze Mheshimiwa Sylivia kwa umahiri na uhodari wake wa kufuatilia masuala ya wavuvi hasa vijana wa Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya mafunzo na uwezeshaji wa makundi haya ya vijana yaliyokwisha kuanzishwa, tunacho chuo chetu cha uvuvi kilichopo pale Kigoma Mjini kwa maana ya Kibirizi, nataka nimhakikishe ya kwamba tutahakikisha chuo kile kinayafikia makundi yote haya, namuomba Mheshimiwa Mbunge aniwasilishie vikundi vile vya Ziwa Tanganyika kimoja baada ya kingine tutakifia kwa mafunzo na tutakifikia katika kukiwezesha hasa kupata mashine ya boti, hilo ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni juu ya kuongeza mikopo kwa tasnia hii ya uvuvi. Serikali hususani Wizara ya Mifugo na Uvuvi tulifanya jitihada ya makusudi ya kuanzisha Dawati la Sekta Binafsi na sasa limefanya kazi kubwa kabla ya kuanzishwa kwa Dawati la Sekta Binafsi Idara ya Uvuvi ilipata mikopo sawa na sifuri kwa wavuvi wadogo na baada ya kuanzishwa tumeipandisha mpaka kufikia milioni 560.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote wanawakilisha wavuvi katika Bunge hili Tukufu kwamba mkakati wetu ni kuimarisha zaidi Dawati la Sekta Binafsi kimkakati, kwa ajili ya kuweza kuiwezesha sekta hii iweze kupata pesa zaidi, maandiko ya vikundi hivi vya wavuvi tutayapitia na kuyawezesha yaweze kuweza kushawishi benki kuweka pesa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini na mkakati wetu wa pili ni bima ya wavuvu; pamekuwa na mgogoro wa muda mrefu juu ya kuweza kupata bima kwa ajili ya wavuvi na wafungaji. Dawati la Sekta Binafsi tumefika mahala kuzuri hivi sasa Shirika letu la Bima la Taifa linakwenda kutupelekea kupata bima ya wavuvi na bima ya mifugo ili sasa mabenki yaweze kuwa na appetite ya kutoa pesa zaidi, ahsante sana. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, shamba hili la Nangaramo lilianzishwa mwaka 1986 wakati Wilaya ya Nanyumbu ikiwa chini ya Halmashauri ya Wilaya ya Masasi. Ukubwa wa shamba hili ni hekta 5,633; hivi ninavyozungumza kuna ng’ombe 300 tu; vijiji vinavyozunguka shamba hili vina uhaba mkubwa wa mahali pa kulima; vijiji vya Kata ya Kamundi, Mkolamwana, Kamundi na Chekereni vina shida kubwa ya mahali pa kulima hata Kata ya Nangomba, Vijiji vya Nangomba na Mji Mwema vina shida kubwa ya mahali pa kulima.

Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri; je, haoni wakati muafaka umefika maeneo haya ambayo hayatumiki kwa shughuli za mifugo wakaruhusiwa wananchi wanaozunguka vijiji hivi wakalima mazao ya muda mfupi, pale ambapo mtakapokuwa tayari basi mnaweza mkayachukua maeneo yenu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; mwaka 2018 kulikuwa na mgogoro mkubwa kati ya wanakijiji cha Mkolomwana na shamba hili, hali iliyopelekea kijana mmoja kupoteza maisha Bwana Ahmad Swalehe na vijana 36 kupelekwa mahakamani. Kwa kuwa kesi ile imekwisha na vijana wale wameachiwa huru kutokuwa na hatia katika mgogoro huu; nini hatma ya kijana huyu marehemu ambaye amepoteza maisha yake kwenye mgogoro huu, je, Serikali ipo tayari kumlipa fidia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahya Mhata kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, namuelewa Mheshimiwa Mhata na juu ya jambo la mahitaji ya wananchi wa kata na vijiji alivyovitaja vinavyozunguka shamba letu la Nangaramo. Naomba nichukue jambo hili kwa niaba ya Wizara, tutakutana na Mheshimiwa Mhata na tuweze kukubaliana kwenda katika eneo hili la Nangaramo na kuhakikisha tunakwenda kufanya tathmini ya kuona hiki anachokisema na kuzungumza na wananchi na pale itakapoonekana inafaa tunaweza tukaona namna ya kuweza kuwasaidia wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni hili linalohusu marehemu huyu; jambo hili ni kubwa, naomba nilichukue, atueleze vyema na sisi tutafanya mashauriano ya kuona namna iliyo bora ya kuweza kulimaliza suala hili, ahsante sana. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwa majibu haya Mheshimiwa Waziri ni wazi kwamba suala la ujenzi wa bandari na ununuzi wa meli katika Mkoa wa Mtwara bado. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza; kwa kuwa wavuvi ili waweze kutengeneza vyombo vyao, wanahitaji kununua miti ama mbao kutoka kwa wauza mbao ambao TFS wanatoa kibali kwao. Nataka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inawapa vibali wavuvi ili waweze kukata ile miti na kutengeneza vyombo kuepusha gharama inayopatikana kwa kwenda kununua kule kwa wauza mbao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa kuwa hakuna uelekeo wa sasa hivi wa kuonekana kutajengwa Bandari ya Uvuvi pamoja na ununuzi wa meli katika Mkoa wa Mtwara, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha inawawezesha wavuvi wa Mtwara kupata vyombo vya kisasa vile vya fibbers nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ni upatikanaji wa mbao na kwa kuwa vibali vinatoka TFS, Wizara ya Maliasili na Utalii, naomba nichukue rai hii ya Mheshimiwa Mbunge na nataka nimhakikishie yeye na wavuvi wote ya kwamba ndani ya Serikali tutalizungumza jambo hili ili kuweza kuona unafuu wa hao wavuvi ambao wanahitaji mbao 10 hadi 15 waweze kuzipata kwa urahisi kwa ajili ya ku-repair au kutengeneza vyombo vipya kwa kuwa ikizingatiwa wao hawaendi kufanya biashara bali wanakwenda kutengeneza vyombo kwa ajili ya matumizi yao. Kwa hivyo, hili ni jambo jema na nalichukua kwa ajili ya utekelezaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni suala la upatikanaji wa fibbers. Tunaanzisha upya Shirika letu la TAFICO na moja ya hadidu za rejea za kuhakikisha TAFICO mpya iweze kufanya vyema ni kuingia ubia kwa maana ya PPP na Sekta Binafasi na moja ya jambo tutakalokwenda kulikazania kwa huyo mtu atakayekuja kwa ajili ya PPP ya ubia ni kuhakikisha atuoneshe dalili na matumaini ya pamoja na kuvua lakini upatikanaji wa vyombo kuanzia katika ukanda wetu wote wa bahari hata na visiwani pia vilevile kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa samaki kwa kutumia vyombo vipya vya kisasa na hii ni pamoja na Mkoa wa Mtwara.
MHE. VINCENT P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuweza kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Nkasi ina kadiriwa na changamoto kubwa sana ya maji, ni lini Seikali itatoa maji Ziwa Tanganyika ambacho ndiko chanzo kikuu cha uhakika kuweza kutatua changamoto Wilayani Nkasi?

Swali la pili; Wilaya ya Nkasi katika Tarafa ya Nkate upo mradi wa maji ambao umekaa muda mrefu sana Tarafa ya Nkate ambao unahudumia vijiji vya Ntuchi, Ntemba, Siriofu na Ifundwa, mradi huu Mkandarasi hajalipwa ili aweze kumaliza mradi huu na ipo kesi ambayo anatuhumiwa mahakamani, naomba Wizara hii iweze kushughulikia kesi ya Mheshimiwa Felix Mkandarasi atoke ili aweze kumalizia mradi huu umekaa muda mrefu wananchi wanahangaika na maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbogo Mbunge wa Nkasi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, lini Serikali itatumia maji ya Ziwa Tanganyika kwa ajili ya kulisha katika Mji wa Nkasi wote. Serikali ya Awamu ya Sita katika vipaumbele vyake cha kwanza ni kuhakikisha kumtua ndoo kichwani mwanamama, kwa hivyo nataka nimhakikishie kazi kubwa imefanyika katika maji eneo la Ziwa Victoria kuyatoa na kuyapeleka Mikoa mbalimbali ikiwemo Tabora na kwingineko, kwa sasa kwenye bajeti hii ya 2021/2022 Serikali inaendelea kutafuta fursa ya kuona namna ya kuweza kusaidia na kwa hivyo hili la Ziwa Victoria naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge linaweza kuwa ni moja ya sababu ya kuweza kulifanyia kazi ili kuondosha hii adha inayowapata wananchi wa Nkasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili juu ya mradi uliokwama wa Kata ya Nkate jambo hili naomba nilichukue na mara baada ya kikao hiki kuisha tuje tulizungumze tulielewe tatizo lake ni nini na baadaye tuweze kulitatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Nimshukuru pia kaka yangu, Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa majibu mazuri yanayoridhisha na kutia moyo. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa kuwa kipato hicho ni kidogo, Serikali ina mpango gani wa kuongeza pato hili kwa pande zote mbili za Muungano na kuwasaidia wavuvi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa kuwa mgawanyo wa mapato ni wa kisheria, je, Wizara inawasaidiaje wavuvi kutoka Zanzibar wanaoleta samaki bara na wale wanaopeleka mifugo Zanzibar ili kuondoa kero na usumbufu unaowapata? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni jitihada gani za Serikali zinafanywa kuongeza pato hili kwa kuwa pato hili ni dogo. Kwanza naomba nimweleze Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote na Watanzania kwa ujumla, natoa shukrani nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, Mama Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nane, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, kwa kuridhia mabadiliko ya sheria na kanuni ambazo zimekwenda sasa kufungua mwanya wa uwekezaji zaidi katika uvuvi wa bahari kuu. Hivi ninavyozungumza, tayari makampuni takribani 20 yameshakata leseni na kuingiza pato la zaidi ya shilingi bilioni moja kwa Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu; ni jitihada kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada nyingine ambayo Serikali hizi mbili zimefanya ni kuhakikisha kwamba tunaweka kipengele ya uvutiaji kwa maana ya incentive. Tumeshatoa maelekezo kwa Mamlaka yetu ya Uvuvi wa Bahari Kuu kuitisha kikao ambacho kitatusaidia kuwaunganisha wadau wote kwa lengo la kwamba tuvitambue sasa vile vivutio ambapo tutawapa Waheshimiwa Mawaziri wawili; wa Jamhuri na yule wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, waweze kuvitangaza hadharani ili wawekezaji wajue iko fursa gani ya kuweza kuwekeza zaidi katika uvuvi wa bahari kuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, baada ya hili la kuongeza kipato, ni nini tunafanya kuondoa vikwazo. Mambo makubwa mawili yanafanyika; hivi sasa timu zetu za wataalam kutoka Zanzibar na kutoka Bara zinakaa pamoja kujadili mambo makubwa mawili; la kwanza, ni leseni za wavuvi wa Zanzibar ziweze kufanya kazi hata huku Bara pia, lakini la pili ni kuondoa kikwazo kile cha mifugo inayotoka Bara kwenda Zanzibar na kulipiwa ushuru mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tupo katika hatua nzuri baada ya Wakurugenzi hawa kumaliza, watakaa Makatibu Wakuu na baadaye watakaa Waheshimiwa Mawaziri ili kufanya harmonization ya sheria hizi na hatimaye Watanzania wote wa Bara na Visiwani, waweze ku-enjoy rasilimali za Taifa letu. (Makofi)
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Wilaya ya Igunga ni wilaya moja wapo inayoongoza kwa mifugo mingi sana hapa Tanzania, je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza idadi ya majosho, hasa Jimbo la Manonga, kutoka majosho matatu hata angalau kufika majosho kumi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika siku 100 za Mheshimiwa Rais, mama Samia Hassan Suluhu, tumemuona akikutana na Mwanamfalme wa Saudi Arabia na wamejadili juu ya masuala ya mifugo, hasa kuuza mifugo lakini pia kuuza nyama nje ya nchi. Je, Wizara imejipangaje kutumia fursa hii; mkakati wake ni upi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Seif Khamis Said Gulamali, Mbunge wa Manonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ni kuongeza idadi ya majosho katika Jimbo la Manonga. Naomba tu nipokee ombi hili la Mheshimiwa Mbunge na nimuahidi kwamba Wizara italifanyia kazi kwa kusudi la kuongeza idadi ya majosho.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni hili la mkakati wa Serikali juu ya kuongeza biashara ya nyama na mifugo nje ya nchi. Kwanza nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan; katika siku hizi 100 moja ya Wizara ambazo amezifanyia kazi kubwa ni hii Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi. Naomba tu nimhakikishie
Mheshimiwa Mbunge ya kwamba Wizara imejipanga vyema kuhakikisha kwamba fursa hii ya kuuza nyama na mifugo nje inatumika na inatumika ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, ni kwa kupunguza kodi mbalimbali ambazo zilikuwa ni kikwazo. Lakini pili, ni kuendelea kushirikiana vyema na sekta binafsi ili kuweza kushamirisha biashara ya mifugo. Na mwisho, mkakati wetu wa kopa ng’ombe lipa ng’ombe, kopa mbuzi lipa mbuzi, tutaupa kipaumbele sana ili kuongeza uzalishaji katika nchi. Ahsante sana.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga soko kuu la kuuzia samaki kwa Mkoa wetu wa Tanga na ni lini ujenzi utaanza?

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili; ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wavuvi wa maeneo ya pembezoni kwa maeneo ya Moa, Chongoleani, Kipumbwi na Mkoaja kuuza samaki wao kwenye soko la pamoja kukwepa wachuuzi kuwachuuza kwa bei ndogo? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Tanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika majibu ya msingi nimeeleza kwamba kwenye bajeti ya mwaka huu na kupitia ufadhili wa Shirika la IFAD, upo mpango wa Serikali wa kujenga masoko ya samaki. Na soko hili litajengwa katika Wilaya ya Pangani katika Kijiji cha Kipumbwi litakuwa ni soko zuri kubwa na la Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ameuliza je watauzia wapi wavuvi wa Chongeleani, Mkinga, Kipumbwi na kwingineko. Naomba nimhakikishie kwamba soko hili litakapokuwa tayari, wavuvi wa maeneo yote aliyoyataja watafaidika kwa ajili ya kuuza bidhaa zao, ahsante sana.
MHE. FELISTER D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, wavuvi wengi wadogowadogo katika ukanda wa Pwani Jimbo la Kawe hasa katika Kata za Msasani, Kawe, Mbweni na Kunduchi wanachangamoto kubwa ya mtaji wa kununua vifaa vya kisasa stahiki ambavyo vinaweza kuwasaidia kupata samaki kulingana na taratibu za kisheria. Ni nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha wavuvi hawa wanapata vifaa hivyo? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza kutoka kwa Mheshimiwa Njau kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mtaji kwa wavuvi ni moja ya Sera yetu ya Serikali na Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan imesisitiza katika kuweka mazingira rafiki ili kusudi wavuvi wetu waweze kupata mikopo.

Mheshimiwa Spika, katika hili, kwa kutumia dirisha lililopo Benki yetu ya Kilimo, iko mikopo kwa ajili ya wavuvi na wadau wanaoshughulika na masuala ya uvuvi.

Mheshimiwa Spika, naomba nimuombe Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine wote wanaotoka katika maeneo ya wavuvi kuhakikisha kwamba wavuvi wanakaa katika vikundi. Na sisi tupo tayari kwenda kuwaunganisha na mabenki na hata kuwapa elimu na mpango mkakati wa namna ya kuandika kuweza ku-access fursa ile ya kupata mikopo, ahsante sana.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kabla ya kuuliza maswali, naomba niishukuru Serikali kwa kunipatia injini siku ya leo Kata ya Kabwe, ninawashukuru sana. Nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: - (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Naibu Waziri amenukuu Ilani ya Chama Cha Mapinduzi Ibara ya 43(h), natambua kwamba Ilani hiyo haijasema tukawatie umasikini Watanzania/wavuvi, imeelekeza mkawapatie mitaji na mikopo. Watu wa Nkasi shida yetu sio Ilani ila Ilani isipotekelezwa hapo ndipo maswali yanakuja. Ni lini Ilani Ibara ya 43 itatekelezwa Wilaya ya Nkasi kwa kuwapatia mikopo wavuvi wa Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kupitia Ilani hiyohiyo, nimesoma mwanzo mpaka mwisho hakuna sehemu Ilani imesema tukawape umasikini Watanzania. Kwa kuwa baada ya operesheni ya uvuvi haramu, Watanzania hasa wavuvi wa Nkasi wamekuwa maskini. Ningependa kujua, nini mkakati wa Serikali kwa kuwapatia vifaa vya kisasa ili kuwaondoa wavuvi hawa katika umasikini. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aida Khenani kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, la kwanza; ninapokea shukrani kwa niaba ya Serikali na Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi uliyoitoa Mheshimiwa Aida Khenani kwa kuwawezesha wavuvi wa Kikundi cha Ushirika cha Kabwe.

Mheshimiwa Spika, lini tutatoa mitaji? Naomba Mheshimiwa Mbunge yeye na wataalam wetu waliopo kule Halmshauri ya Nkasi kwa pamoja tushirikiane katika kuhakikisha kwamba tunaandaa sasa utaratibu wa vikundi hivi kuweza kupata fomu, kuzijaza, waainishe, wapewe elimu kwa kusudio la kuweza kuwaunganisha na Benki ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Aida Khenani, nipo tayari kabisa kuhakikisha kwamba tunasimamia jambo hili katika kutekeleza Ilani makini kabisa ya Chama Cha Mapinduzi ili kusudi wananchi hawa waweze kupata mikopo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili; ni kwa namna gani tutawasaidia mara baada ya kufanya operesheni ambayo yeye Mheshimiwa Mbunge anaitamka kwamba imewatia umasikini. Nataka nikuhakikishie kwamba kwanza operesheni ile ilikuwa ni kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi na matokeo ya operesheni ile wengi wameyavutika kwa sababu tulipata samaki wengi, wakubwa na wazuri.

Mheshimiwa Spika, na sasa namna ya mpango tulionao wa namna ya kuwasaidia, moja ni hili tulilolifanya leo kwa kukukabidhi mashine itakayokwenda kuwasaidia watu wa kule Kabwe. Na ninakupa hamasa wewe na Wabunge wengine wanaotoka katika kanda ya uvuvi watuletee maombi zaidi ili kusudi Serikali tuweze kusaidiana nao. Na dirisha la Benki ya Kilimo liko wazi, sisi tunacho kitengo maalum cha kuweza kusaidiana na wavuvi kuandika programu zile na kwenda kuomba zile pesa ili waweze kununua zana bora na waweze kufika mahala mbali kunapoweza kuwasaidia kupata mavuno toshelevu na biashara nzuri, ahsante sana.
MHE. NORA W. MZERU: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri kutokana na migogoro ya muda mrefu, baina ya wafugaji na wakulima nchini hususani Mkoa wangu wa Morogoro. Je, Serikali itawasaidiaje wafugaji maeneo ya malisho ili kuepusha migogoro na wakulima? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nora Waziri Mzeru Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, migogoro ya wakulima na wafugaji katika Mkoa wa Morogoro, tunayo Ranch yetu ya Taifa ya Mkata. Tumekwisha kuanza utaratibu wa kuwagawia wafugaji wenyeji wa Mkoa wa Morogoro. Hadi sasa tumeshatoa vitalu saba, kwa ajili ya wafugaji katika eneo hili na utaratibu huu unaendelea. Pia, Wizara inayo mkakati wa maeneo yake ambayo tumekubaliana kwamba, yako chini ya kiwango cha matumizi ikiwemo baadhi ya Ranch LM News na Holding Grounds. Hizi zote tunazitazama na kuhakikisha kwamba tutazipima na kugawa vitalu baadhi kwa wafugaji walioko maeneo mbalimbali nchini. Ili kuweza kuwasaidia kuondokana na hamahama na kwenda kugombana na wafugaji na wakulima. Ahsante sana.
MHE. VINCENT P. MBOGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Uchumi wa blue unafanana na mazingira mazuri kabisa sawa sawa na Ziwa Tanganyika. Je, Serikali ina mpango gani kama inavyofanya kwenye mazingira ya Bahari ya Hindi rasilimali zinavyopatikana baharini, vivyo hivyo na rasilimali zinapatikana Ziwa Tanganyika. Ni lini Serikali mnakuja na mkakati maalum swali namba moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili dagaa Ziwa Tanganyika ni zao la kipekee ambalo ndio linasababisha uchumi wa Mikoa mitatu Kigoma, Rukwa na Tanganyika. Serikali ina mpango gani na zao hili na pia kwa sababu linavuliwa ndani ya Mikoa mitatu, libadilishwe jina sio dagaa wa Kigoma waitwe dagaa wa Ziwa Tanganyika ili kuweza kutangaza Ziwa Tanganyika? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua kwanza fursa hii, kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbogo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, la kwanza naomba kwa namna ya kipekee nimpongeze yeye na Wabunge wote wa Mkoa wa Kigoma, Katavi na Rukwa kwa kuona umuhimu wa Ziwa Tanganyika na mazao yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Rais Samia Suluhu Hassan, moja ya mkakati ni hili la uchumi wa blue na ni kipaumbele kama Taifa letu na ndio maana katika bajeti ya mwaka huu, Serikali ya Awamu ya Sita imeweka jumla ya kiasi cha shilingi milioni 800. Kwa kusudio la kwanza ni kuhakikisha kwamba tunafanya stock assessment. Ziwa Tanganyika halijawahi kufanyiwa stock assessment kwa mara ya kwanza sasa tunakwenda kufanya stock assessment, ya kujua ni kiasi gani cha Samaki migebuka na dagaa tulionao katika eneo lile. Hii itatusaidia sana kwenye mkakati wa uchumi wa blue, ili kuweza kuvutia uwekezaji na watu kuweza kujua kwamba akiweka fedha yake itakwenda kumlipa kwa kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hili la pili la ushauri la kwa nini dagaa hawa wasiitwe dagaa wa Ziwa Tanganyika? Nataka nimhakikishie yeye na Waheshimiwa Wabunge wote tumeuchukua ushauri huu. Isipokuwa kibiashara wewe unafahamu ya kwamba katika marketing strategy dagaa hili limetambulika kwa miaka mingi sana kama dagaa la Kigoma.

Kwa hiyo, ikiwapendeza sisi tutakaa nao tutashauriana nao badala ya kuwa dagaa la Kigoma, tutasema kwamba liitwe dagaa la Tanganyika. Kwa dhumuni jema lile la kwamba wanavuliwa kwenye Mikoa yote mitatu, Rukwa, Katavi na Kigoma kwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na dagaa hizi ni mali sana hazijawahi kushuka bei hivi sasa inauzwa mpaka shilingi 30,000 kwa kilo na haijawahi kushuka chini ya shilingi 20,000. Ahsante sana.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Ziwa Tanganyika linatumika zaidi ya nchi moja kwa maana ya Tanzania kuna Congo, Burundi na nchi nyingine. Lakini dagaa wengi wanapatikana Ziwa Tanganyika upande wa Tanzania na sheria ambazo mlizitunga pamoja na Kanuni, zinawa-guide wavuvi wa Tanzania wavue usiku wakati dagaa wengi wanapatikana mchana. Kwa hiyo, ni muda muafaka sasa wa Wizara ya Uvuvi hawaoni kwamba, kuendelea kutumia hizo sheria ambazo zinawakandamiza wavuvi wa Tanzania na kuwapa faida nchi nyingine waachane nazo? (Makofi)

SPIKA: Kwa hiyo, kule Congo na wapi wanavua mchana?

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, ndio wanavua mchana.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumepokea malalamiko na tumepokea mapendekezo ya wavuvi wote wa Ziwa Tanganyika na hivi sasa, Wizara inafanyia kazi mapendekezo haya yote yaliyotolewa na wavuvi. Lakini naomba kwa ruhusa yako kwa sekunde moja. Dagaa ni aina tofauti katika miongoni mwa aina za samaki tulizonazo, mle katika Ziwa Tanganyika tunao dagaa, tunao migebuka. Lakini Ziwa Tanganyika ni maarufu zaidi kwa samaki wa marembo wanaouzwa duniani kote na tunapata mapato makubwa sana kama Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa nini usiku? Tunaweka sayansi inayoelekeza tunapovua usiku dagaa tunaweka light attraction, ni dagaa pekeyake ndiye anayeweza kuvutwa na mwanga wa taa. Migebuka havutwi, samaki wa marembo havutwi, sangara havutwi anayevutwa ni dagaa peke yake.

Sasa, tunafanya vile kuwavuta dagaa ambao wanakuja katika mtindo wa makundi kwa maana sculling, ili kuwaepusha kuchukua samaki wa aina nyingine. Sasa hawa wanaovua mchana, nina hakika siwezi kuzungumzia nchi zingine, lakini hapo nimezungumza from scientific point of view.

Mheshimiwa Spika, ni kwa nini msingi wa kwa nini tunasema usiku na dagaa asivuliwe mchana, ukimvua mchana utavua na migebuka, utavua na samaki wengine wasiohitajika. Kwa sababu, kila leseni anayopewa mvuvi anapewa kwa kusudio maalum. Lakini hiyo tumeichukua hoja hii na sisi kama wataalam tupo katika harakati za kuangalia, ili tuweze kuendana na mahitaji ya wavuvi wetu waweze kunufaika na rasilimali hii. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Awali ya yote naomba niipongeze Serikali na Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kutupatia vifaa boti katika Jimbo letu la Mchinga. Sambamba na kutupatia mashine katika Jimbo letu la Mchinga na sasa hivi wako kwenye mchakato wa kutupatia hiyo boti. Halikadhalika wako kwenye mchakato mwingine wa kutujengea eneo ambalo wavuvi hawa wadogo wadogo hasa katika Jimbo langu la Mchinga, watajenga mwalo ili wavuvi wote wawe na sehemu ya uhakika ya kuuzia bidhaa zao kutoka kwenye Bahari yetu ya Hindi. Swali langu ni hili lifuatalo: - (Makofi)

Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itaanza ujenzi huu wa mwalo katika Jimbo langu la Mchinga na hasa Kata ya Mchinga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mama yangu Salma Rashid Kikwete, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana ni ukweli kwamba Serikali ya Awamu ya Sita ya Rais Samia Suluhu Hassan imepeleka mashine za kutosha. Lakini vile vile na Kamba ambazo zilikuwa ni maombi ya kwake yeye mwenyewe Mbunge wa Jimbo la Mchinga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na katika hilo pia vile vile Serikali ya Awamu ya Sita imetenga jumla ya shilingi milioni 800, kwa ajili ya kujenga Mwalo na sasa hivi tupo katika hatua tayari kwa pamoja kwa kushirikiana na wananchi wa Mchinga, tumeshachagua eneo litakalokwenda kujengwa ule mwalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sasa tupo katika michoro na baadaye kupata BOQ ambapo jumla ya kiasi cha fedha kisichopungua Shilingi milioni 800 zimetengwa kufanya kazi hiyo. Ninaamini kazi hiyo itakapokamilika ndani ya mwaka huu wa fedha itawanufaisha wavuvi wa eneo hili la Mchinga na wengine katika Pwani ya Bahari ya Hindi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri yanayotia moyo. Lakini katika sentensi yake tu ya kwanza amesema ile ni Benki ya Maendeleo ya Kilimo na mimi nazungumzia wavuvi.

Sasa ninataka kujua, je, ni vigezo gani vinavyotumika ili hao wavuvi waweze kupata mikopo katika hiyo Benki ya Kilimo?

Swali la pili; ninataka kujua, kwa kuwa wavuvi wengi bado hawajapata elimu kuhusiana na mikopo hiyo; Je, Serikali ina mpango gani wa kuzungukia wavuvi hao ili wapate elimu waweze kunufaika na mikopo hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza kuhusu ni vigezo gani. Kwanza ni kuomba ama kama nilivyoeleza katika jibu la msingi, mtu mmoja ama kikundi, waombe kwa watoaji wa mkopo kwa maana ya benki. Tunashauri vikundi, hasa vya ushirika kwa kuwa ni rahisi zaidi kulingana na sera yetu kupata mkopo kisha benki watakapokuwa wameombwa wataeleza nini kimepungua na nini kinachohitajika ili mwombaji aweze kukamilisha utaratibu. Kwa hiyo namshauri Mheshimiwa Malembeka na wavuvi wote kutembelea katika mabenki mbalimbali na wanaweza kupata msaada wa kuelezwa ni nini hasa vile vigezo vinavyohitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili la utoaji wa elimu ni endelevu na limekuwa likiendelea kufanywa wakati wote, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Malembeka ya kwamba tutaendelea kufanya kazi hii ya kutoa elimu kwa wavuvi wetu juu ya uvuvi endelevu katika Taifa letu na wenye manufaa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo ya nyongeza, lakini kabla sijauliza maswali yangu madogo kuna kumbukumbu naomba kuiweka kwa usahihi kuhusiana na suala zima la ushuru na tozo za minada ya mifugo katika Wilaya ya Longido tulipata heshima kubwa ya kutembelewa na Rais kama wiki mbili zilizopita tarehe 18 na kuna Waandishi wa Habari ama wamempa Rais habari ambayo siyo sahihi, baada ya kufungua kiwanda kikubwa cha nyama ambacho kimezinduliwa kilijengwa na wawekezqji kwa zaidi ya shilingi bilioni 17 akapata taarifa kwamba inazalisha chini ya kiwango kwa sababu Halmashauri ya Wilaya ya Longido inatoza kodi na ushuru mkubwa unaosababisha wafugaji kupeleka mifugo Kenya.

Mheshimiwa Spika, kumbe Halmashauri ya Wilaya ya Longido haijawahi kuchukua hata shilingi katika kile kiwanda tangu kianze na kodi zinazokusanywa zinaenda Wizarani na taarifa hiyo ilitoka katika taarifa ya Ikulu wananchi wa Longido walikereka sana na hiyo kauli, nikaomba sasa basi nitoe hapa wasikie kwamba nimewasema na ndipo sasa niulize maswali yangu mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza kwa kuwa viwanda hivi vilivyojengwa nchini hivi karibuni vya kisasa ikiweko hicho cha Eliya Food Products kilichoko Longido zinapata malighafi pungufu kulingana na uwezo wake.

Je, Serikali imeweka mpango na mkakati gani wa kuhakikisha kwamba malighafi ya kulisha hivyo viwanda inapatikana?

Swali la pili; kwa kuwa Wilaya ya Longido ni Wilaya ya wafugaji kwa asilimia 95 na afya ya mifugo inategemea kwa asilimia kubwa upatikanaji wa maji hasa maji ya mabwawa - malambo yale.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuyafufua mabwawa na malambo yaliyofukiwa na udongo kwa miaka mingi katika Wilaya ya Longido na hasa Kiseriani ambapo maji kidogo yaliyobaki mwaka huu yanakwamisha wanyamapori? Juzi nimeweka post ya Pofu aliyekuwa anatolewa na Wamasai amekwama katikati ya lile bwawa pamoja na binadamu, sisi tunatumia maji ya mifugo na binadamu pia.

SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Kiruswa..

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Wizara ya Maji inawahusu mtatusaidiaje kufufua mabwawa yaliyofukiwa katika Wilaya ya Longido?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Stephen Kiruswa Lemomo Mbunge wa Longido kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza linahusu mkakati wa Serikali wa kuhakikisha viwanda hivi vinapata rasilimali, tumejipanga juu ya kuhakikisha tunaweka utaratibu wa unenepeshaji kupitia vikundi na kwa watu binafsi. Mkakati wetu ni kuwa na wanenepeshaji wasiopungua 500 nchi nzima ambao miongoni mwao watakwenda kuingia mikataba na viwanda, kwa mfano kiwanda cha Eliya Foods kimeshaanza utaratibu huo wa kuwa na suppliers ambao wanawapa mikataba kwa ajili ya kupeleka ng’ombe pale kiwandani na hii itatusaidia sana hata katika lile jambo la mwanzo alilolizungumza la tozo kwa kuwa utaratibu tuliouweka wale wote watakaokuwa na mikataba na viwanda vinavyofanya uchakataji kwa ajili ya export tutawaondoshea baadhi ya tozo hizo ili kurahisisha vile viwanda viweze kupata malighafi kwa urahisi na kwa bei nzuri.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni hili la maji katika bajeti ya mwaka 2021/2022 tunayo malambo ambayo tunayatengeneza kwenye maeneo mengine ya nchi hii, lakini nafahamu Longido uko mradi mkubwa wa maji ambao unakwenda kuwahudumia wananchi wa Longido. Tumekaa na wenzetu wa Wizara ya Maji na nimpongeze sana yeye Dkt. Kiruswa na timu nzima ya pale Longido Mkoani Arusha kwa kuwashawishi wenzetu wa Wizara ya Maji waweze kutoa matoleo ambayo yatatengeneza mabirika yahudumie mifugo na wakati huo huo yaweze kuhudumia wanadamu na sisi ndani ya Serikali tunaendelea na ushauriano ili kusudi jambo hili liweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, hivyo mradi ule mkubwa wa maji uliokwenda kuzinduliwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan wa kuhakikisha kwamba uweze kuhudumia maji haya yaweze kuhudumia binadamu na mifugo pia. Ahsante sana.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa nilitaka niongezee jibu sehemu ndogo ili Mheshimiwa Mbunge ambaye anawasemea sana wananchi wa Longido aweze kulibeba hilo jibu. Wizara ya Fedha pia kushirikiana na Wizara ya Mifugo tunaangalia upya sehemu ya tozo ile ambayo tuliiweka ambayo inahusu pia sekta ya mifugo pamoja na maeneo mengine ambayo yamesababisha upande wa huku Serikali Kuu iweze kuongeza hiyo sehemu ambayo ameisemea, kwa hiyo naamini kwenye kikao hiki hiki kinavyoendelea tukiwa tumeshakamilisha Mheshimiwa Mbunge atarudi Longido akiwa na jibu lililosahihi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu sehemu ya kufufua bwawa tayari tumeshakamilisha makubaliano na Waziri wa Maji ambaye anafanyakazi nzuri sana, tumeshatoa fedha za kununua mitambo ya kuchimba mabwawa ambako kila ukanda wa nchi hii utakuwa na mtambo wake wa kuchimba mabwawa. Kwa hiyo kwa wafugaji hata kama wataamua kuchimba bwawa kila baada ya mazizi mawili Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wetu amesema wachimbe tu na wata-manage wenyewe kutoa maeneo ya kuchimba hayo mabwawa. (Makofi)
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa kwa muda mrefu wavuvi wadogo wadogo kutoka katika Wilaya ya Kilwa na maeneo mengine ya nchi yetu ya Tanzania wamekuwa hawapati mikopo kutoka kwenye mabenki kwa ajili ya kufanyia shughuli zao mbalimbali za kuboresha shughuli za uvuvi.

Je, Serikali haioni sasa wakati umefika wa kuweza kuwaundia hawa wavuvi wadogo wadogo mfuko maalum ambao wataweza kukopa kwa riba ndogo na hatimae hiyo mikopo iweze kuwanufaisha katika kufanya shughuli zao za uvuvi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Wilaya ya Kilwa kumekuwa na wimbi kubwa la uingiaji wa wafugaji wenye mifugo mingi sana hasa katika Kata za Somanga, Tingi, Kandawale, Njinjo, Mitole, Likawage, Nanjilinji pamoja na Kikole.

Je, Mheshimiwa Waziri ni lini atafika katika Wilaya ya Kilwa ili kuwasaidia wananchi wa Wilaya ya Kilwa kwenda kutatua changamoto mbalimbali zinazotokana na uingiaji wa mifugo mingi katika Wilaya ya Kilwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ndulane Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya kuanzishwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Uvuvi kwa ajili ya kuwasaidia wavuvi wadogo wadogo waweze kupata mikopo ya bei nafuu na yenye riba ndogo. Ninaungana na yeye na ninampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa niaba ya Wabunge wote ambao wanasimamia wavuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa miaka mitano tulionao Wizarani mwaka 2021-2016 wa kuhakikisha tunaupa nguvu uchumi wa blue, jambo hili la kuanzishwa kwa Fisheries Development Fund (Mfuko wa Maendeleo ya Uvuvi) ni miongoni mwa jambo lililopewa kipaumbele. Kwa hivyo, Mheshimiwa Mbunge nikupongeze kwamba umelileta jambo ambalo tayari Serikali imeshaliona na kwa hivyo tunakwenda kulianzisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili la kuingia kwa mifugo. Tayari tumekwenda kufanya ziara na nimpe pole sana yeye na wananchi wote, lakini tumekwenda na tumezungumza na makundi mbalimbali, katika Wilaya ya Kilwa nilifika katika Kata ya Nanjilinji kwenda kuzungumza na wananchi pale lakini niko tayari kurejea tena ili kusudi tuweze kufika kule kote alipotaja Mitole, Njinjo, Likawage, Kandawale na hata kule Miguruwe na Zinga Kibaoni, ili kuweza kwenda kuzungumza na wananchi kwa niaba ya maombi haya ya Mheshimiwa Mbunge na hatimaye kuweza kupata suluhu ya tatizo hili kubwa ambalo linawasumbua wananchi wa Kilwa Kaskazini. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, pamoja na kupongeza kazi nzuri sana inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita, chini Rais Samia ya kufufua uchumi wa Mkoa wa Lindi ikiwemo kufufua mazungumzo ya Mradi wa LNG, lakini pia na utengaji wa shilingi billion 50 kwa ajili ya kujenga Bandari ya Uvuvi Kilwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni lini mchakato huu wa ujenzi wa hii bandari ambao ni ukombozi mkubwa wa ukanda wetu utaanza? Kwa sababu ahadi iliyokuwepo ni kwamba mchakato huu ungeanza mapema pamoja na kumshukuru Mama Samia kwa kazi hii nzuri lakini lini mchakato huu utaanza wa kujenga bandari hii kwa ajili ya uvuvi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nape Moses Nnauye Mbunge wa Mtama Mkoa wa Lindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nimpongeze sana kwa swali hili zuri na la kimkakati. Ujenzi wa bandari ya Uvuvi umetamkwa kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020/2025, nasi tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kukubali kwake na msukumo wake wa kuhakikisha kwamba mradi huu wa kimkakati wa ujenzi wa bandari unafanikiwa na hatimye kuweza kwenda sambamba na ile zana ya uchumi wa blue. Tayari wataalamu wetu wameshafanya hatua zote za mwanzoni na imekubalika kitaalamu ya kwamba bandari ile itakwenda kujengwa pale Kilwa Masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa wataalam wapo katika hatua za mwisho kabisa ya kuweza kuli-demarcate kuliweka sawa lile eneo linalokwenda kuwekwa bandari ile. Na tunashukuru sana kwa kuwa eneo hili ni eneo la kimkakati la kuelekea kule katika bahari kuu. Hivyo kile kilio cha muda mrefu cha Wabunge wengi na Watanzania wengi cha kwamba nchi hainufaiki ipasavyo na bahari yetu sasa kinakwenda kupata muarobaini wake. Kwa kweli tunamshukuru Mheshimiwa Rais hata kwa zile pesa za kununua meli nane ambapo sisi Tanzania bara tutapata meli nne zitakazo kwenda kuvua upande wa bahari kuu. Ninashukuru sana. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana, Wilaya ya Hai inawafugaji wengi sana wa ng’ombe wa kisasa, ng’ombe walionenepeshwa lakini pia ng’ombe wale wa kienyeji pia tuna Uwanja wa Ndege wa Kimataifa na tuko tayari kufanya biashara ya Kimataifa ya kuuza nyama.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza machinjio ya kisasa katika eneo la KIA ili na sisi tuweze kufungua milango ya kibiashara ya kuuza nyama?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mafuwe Mbunge wa Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli wafugaji wa Hai ni wafugaji wa ng’ombe wa kisasa wanafuga katika utaratibu ule wa zero grazing, ni katika maeneo yanayofuga vizuri sana na viwanda vidogo vidogo vya maziwa viko pale Hai. Lakini vile vile Hai wanavyo viwanda vya chakula vya mifugo, hongera sana Mheshimiwa Mafuwe na wananchi wote wa Hai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni lini tutajenga machinjio ya kisasa, ninaomba Mheshimiwa Mafuwe wewe na waheshimiwa madiwani wenzako katika Halmashauri ya Hai muanzishe mpango huu, na sisi Wizara ya Mifugo na Uvuvi tutakuwa tayari kushirikiana nanyi katika kuwapa utaalam na mchango mwengine wowote wa kuhakikisha jambo na wazo hili zuri linatimia pale Hai, ahsante sana. (Makofi)
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana, katika jimbo la kawe Kata ya Mbweni kuna wavuvi wengi wadogo wadogo na upatikanaji wa samaki ni mwingi sana lakini wavuvi wele hawana soko la uhakika pale, hawana sehemu maalum ya kuuzia. Ni lini Serikali itajenga soko la uhakika katika Kata ya Mbweni ili kuinua uchumi wa wavuvi wadogo wadogo na kuinua pato la Taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Felisha Njau kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika maeneo ambayo yana wavuvi wengi kwenye Jimbo la Kawe wako wavuvi pia. Hapa karibuni nilikwenda kwenye Beach ya Kawe kwa maana ya Kawe Beach, ambako pale lipo Soko la Wavuvi, tayari tumetoa maelekezo kwa wataalam wetu kwenda kuzungumza na viongozi wa eneo lile wakiongozwa na Mheshimiwa Diwani kijana Mheshimiwa Lwakatare, kwa ajili ya kukaa na wavuvi wale na kupanga mpango tuweze kushirikiana na Hamnashauri ya Wilaya ya Kinondoni ambayo ina mapato mazuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi Wizara ya Mifugo na Uvuvi tutashirikiana nayo kuhakikisha kwamba tunatengeneza soko zuri ni mahali pazuri ambako tunaweza kuvua kutengeneza samaki na watu waweze kwenda pale weekends ku-enjoy samaki wa baharini, ni samaki wazuri sana, ahsante sana. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kwenye majibu ya msingi ya Mheshimiwa Waziri hajaeleza na wala hajaitaja Ranchi ya Ruvu iliyopo pale Vigwaza kama imeshatengwa, sasa kwa kuwa kuna migogoro mingi ya wakulima na wafugaji kwenye Mikoa ya Pwani na maeneo mengine ya jirani kama Wilaya ya Chalinze na Kibaha Vijijini; Je, Serikali haioni huu ni muda sahihi sasa kupanga na Ranchi ile ili kumaliza migogoro ya wakulima na wafugaji kwenye maeneo hayo?

Swali la pili; kwa kuwa Mheshimiwa Waziri anafahamu kwamba migogoro mingi ya wakulima na wafugaji inapelekea watu wengi kupata ulemavu wa kudumu na wengine kufariki na kwa sababu ipo Ranchi hiyo ninayoitaja ya Ruvu ambayo haijafanyiwa; Je, Waziri haoni kwamba ni muda sahihi wa kufika kwenye maeneo ya Mkoa Pwani hasa Wilaya hizo za karibu kuwaelimisha wafugaji wadogo kwenda kuomba na kupata utaratibu wa kukaa kwenye Ranchi hizo kuondoka kwenye Bonde la Ruvu ambalo lina migogoro? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Michael Costantino Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru na kumpongeza sana lakini pili kwanini Ranchi ya Ruvu haikutamkwa katika majibu haya. Ranchi ya Ruvu katika maelekezo ya muda mrefu uliopita ya Serikali haikupangwa kwa ajili ya vitalu vya muda mrefu. Ranchi ya Ruvu na Ranchi ya Kongwa hazikupangwa. Kwa hivyo, baadaye kwa utashi na maelekezo ya viongozi wetu wakuu na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutaka kuona tunatatua changamoto ndiyo uamuzi wa kukata vitalu vya muda mfupi ukafanywa kwa hivyo Ranchi ya Ruvu ikapangiwa ikatwe vitalu jumla ya 19 na hivi sasa ninavyozungumza jumla ya Ng’ombe zaidi ya Elfu Tisa katika vitalu hivi vidogo vidogo vilivyopo katika eneo nzima la Ranchi Ruvu vimeshagawiwa kwa wafugaji, hili ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni namna ya kuweza kuwatoa wale wafugaji walioko katika maeneo ya Bonde la Mto Ruvu na labda kuwapa nafasi huku. Serikali jambo hili inalifanyia kazi siyo peke yake katika Mto Ruvu lakini vilevile na mito mingine kama Kilombelo, Ruaha na mingineyo. Maelekezo ya Serikali ni kwamba iko Kamati ya Mawaziri Nane inayofanya tathmini ili tutakapotoka na majawabu, tutatoka na majawabu ya pamoja yatakayokwenda kutatua kabisa tatizo hili la muda mrefu la wafugaji, wakulima na watumiaji wengine wa ardhi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, nami naomba niulize swali la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri wa Mifugo.

Mheshimiwa Spika, zaidi ya jumla ya hekta 2,208 zimegawiwa kutoka kwenye Ranchi ya Ruvu kwenda kkwetwa wanavijiji vinavyozunguka au katika Halmashauri ya Chalinze vikiwemo vijiji vya Kindogonzelo, Kitonga, Magulumatali, Vigwaza na Milo. Je, ni lini Serikali inakuja kutukabidhi vipande hivyo vya ardhi kwa ajili ya wananchi wetu sasa kuweza kugawana ili kuweza kutengeneza utaratibu mzuri wa kufuga. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa
Spika ahsante sana umetupa elimu nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali zuri la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Chalinze Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Mrisho Kikwete kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli kwamba tumetenga hekta 2,208 hii ni kwa sababu ya lile jibu la msingi nililolitoa lililoulizwa na Mheshimiwa Mwakamo la kuondosha migogoro kati ya wakulima na wafugaji ni moja ya jitihada za Serikali na utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, tayari hatua za mwanzo za kiutawala ndani ya Wizara zimeshafanywa, vimeshapimwa na kutengwa maeneo haya, hatua inayofuata sasa ni kwenda kuwakabidhi Halmashauri ya Chalinze na Kibaha na hasa Jimbo la Chalinze, Jimbo la Kibaha Vijijini na Jimbo la Bagamoyo. Mara tu baada ya Bunge Wizara itakuwa iko tayari kabisa kuhakikisha kwamba sherehe hizi za kwenda kuwakabidhi na waweze kujipangia matumizi zinakwenda kufanyika. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa vile Serikali imetoa majibu mazuri sana, naomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Je, Serikali imefanya tathmini katika elimu inayotoa, kama kusaidia kupunguza uvuvi huu haramu ambao bado tunauona unaendelea?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Maryam Azan Mwinyi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wote tumekuwa tukifanya tathmini na ninakubaliana na Mheshimiwa Mbunge ya kwamba pamoja na elimu tunayoitoa, bado tatizo la uvuvi haramu liko pale pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya Serikali tumekubaliana; la kwanza, elimu ni jambo endelevu, kwa hiyo, tutaendelea nalo. La pili, ni kupanua wigo na kufanya ushirikishaji zaidi ili kusudi tuweze kupambana na vita hii ya uvuvi haramu kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikuhakikishie ya kwamba wavuvi walio wengi wanaelewa sana ya kwamba hiki ni sahihi na kipi kisicho sahihi. Tunazo changamoto za msingi sana ambazo zinawapelekea wakati mwingine baadhi yao; aidha kwa makusudi au kwa au kwa bahati mbaya wanaingia katika vitendo hivi haramu. Miongoni mwa changamoto hizo ni ongezeko la mahitaji ya hizi rasilimali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ya kwamba Serikali tunafanya tathmini na tunaendeleza mikakati ya kuhakikisha tunafanya uendelevu wa rasilimali zetu.
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri ameelezea jinsi gani walivyojipanga kutoa elimu ya kuondoa madhara ya uvuvi haramu; na mara nyingi uvuvi haramu hufanyika kwa vifaa duni na ambavyo siyo sahihi; na vifaa sahihi hupatikana kwa gharama kubwa; na wengi wanaofanya uvuvi haramu ni kwa sababu hawana vifaa vile: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kujua: Je, Serikali ina mpango gani ili kuinua kundi hili la wavuvi wadogo wadogo kiuchumi hasa katika Pwani yetu ya Bahari ya Hindi na Maziwa Makuu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Angelina Malembeka kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze sana kwa kuwa amekuwa kila mara mstari wa mbele kwenye kuwasemea wavuvi hasa wavuvi wadogo wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi, ni kwamba mkakati wetu ni kuendelea kurekebisha sheria zetu na kuziboresha. Hili ni jambo la kwanza ili kusudi ziweze kuendana na wakati, maana wavuvi wamekuwa kila mara wanagundua zana mpya, zana ambazo labda wakati mwingine kwa upande wa sheria zetu tunakuwa nyuma ya teknolojia hizi ambazo wavuvi wamezigundua. Kwa hiyo, huu ni mkakati wetu wa kuhakikisha tunakwenda nao sambamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kurekebisha katika masuala ya kikodi. Tumekuwa tukifanya hivyo kila mara ili zana zetu ziweze kukidhi haja ya wavuvi kwa maana ya bei; na tatu ni mkakati wetu wa kuunda vikundi vya ushirika wa wavuvi na waweze kupata mikopo iliyo na riba nafuu kupitia Benki yetu ya Kilimo na hatimaye kuweza kuwasaidia kwenye kufanya shughuli zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, naomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge, tunayo dhana pana sasa ya uchumi wa blue ambayo tumedhamiria, Serikali ya Awamu ya Sita ya Rais Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kwamba tunahamasisha na kutangaza dhana hii ambapo katika ukanda wote mathalan wa bahari ya hindi tuweze kutumia ipasavyo rasilimali zote zinazopatikana ili kuweza kuwafanya wavuvi wetu wawe na kipato kinachotosheleza kwa ajili ya kaya kwa maana ya familia zao na kuweza kuwa na mchango mpana kwenye pato la Taifa letu.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Wizara tayari imeshaanza utaratibu wa kutoa elimu ya huo uvuvi unaoitwa haramu, miongoni mwa wilaya zilizoathirika ni pamoja na Wilaya ya Nkansi ambao walichomewa nyavu zao kwamba wanavua uvuvi haramu, lakini Serikali haijawahi kuwapatia mbadala wa nyavu zinazoitwa halali. Leo wamejikongoja wachache wameendelea na uvuvi, wanavamiwa na watu kutoka Kongo na Burundi. Wajibu wa Wizara ni kuwalinda wavuvi hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua, mna mkakati gani wa haraka wa kuwasaidia wavuvi hawa ambao wamevamiwa na vifaa vyao bado viko Kongo na Burundi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkansi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni jinai na kwa hiyo, litashughulikiwa katika utaratibu wa kijinai. Naomba kwa kuwa ni jambo mahususi, tuweze kushughulika nalo katika utaratibu wake. Hapa umetaja nchi ambazo ni majirani zetu. Kwa hiyo, unaweza ukaona kwamba ni jambo mtambuka. Hapa umetaja jambo ambalo linaweza kushughulikiwa pia na Wizara, sisi na Wizara ya Mambo ya Ndani ya na kwa sababu linahusisha nchi nyingine na Wizara ya Mambo ya Nchi na Nje na wengine tunaohusika katika masuala ya ulinzi na usalama wa Taifa letu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa uvuvi haramu umeathiri sana mapato hasa kwenye mabwawa mengi, pamoja na Bwawa la Mtera ambapo Halmashauri ya Iringa Vijijini imekuwa ikipata mapato yake.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza mabwawa yawe mashamba darasa kwenye Halmashauri nyingi pamoja na Jimbo la Kalenga ili tuweze sasa kufundisha vijana wengi pamoja na akinamama na akinababa waanze kutegemea uchumi wa kufuga samaki kupitia haya mabwawa ambayo yatakuwa ni mashamba darasa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kiswaga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mkakati wetu. Katika bajeti ya mwaka huu 2021/2022 kupitia mradi wa AFDP kwa maana ya Agricultural Fisheries Development Program II, tumetenga pesa kwa ajili ya kuweza kutengeneza mashamba darasa ya ufugaji wa Samaki. Hapa walengwa ni makundi ya vijana na akina mama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimkaribishe Mheshimiwa Kiswaga ili tuweze kushirikiana katika hatua hii. Yawezekana Wilaya ya Iringa Vijijini kwa maana ya Jimbo lake likawa ni sehemu ya wanufaika. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, Nakushukuru sana na nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina swali moja dogo la nyongeza. Vifo vingi vya mifugo hutokea kipindi cha kiangazi au ukame kutokana na upungufu mkubwa wa maji na malisho ya mifugo hususan mwaka jana mwezi Septemba mpaka Januari mwaka huu vifo vingi vilitokea hasa katika Wilaya ya Kiteto ambapo zaidi ya mifugo 1,874 ilikufa na Simanjiro zaidi ya mifugo 62,500 ilikufa, mabaki Bonde la Magara mifugo ilikufa lakini mifugo ilizidi kudhoofu katika Wilaya ya Mbulu na Hanang.

Je, Serikali sasa haioni umuhimu wa kuwekeza miundombinu wa uhakika ikiwepo wa uchimbaji wa visima virefu, mabwawa na malambo katika maeneo haya kukabiliana na vifo vya mifugo, lakini vile vile, kumnusuru mfugaji asibaki katika dimbwi la umasikini. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UVUVI NA MIFUGO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yustina, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Manyara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nampa hongera Mheshimiwa Mbunge Yustina kwa ufuatiliaji huu wa jambo hili zito lililowapata wafugaji. Mbili, pia atakubaliana nami kwamba Serikali ilitoa pole kwa wafugaji wote wa Mkoa huu wa Manyara ambao ameutaja hapa.

Katika jibu letu la msingi tumeeleza ya kwamba tutafanya mazingatio katika bajeti ya mwaka huu wa 2022/ 2023 ambapo tutachimba visima virefu na vile vile tutajenga mabwawa na kwa msisitizo maeneo haya aliyoyataja yote tutazingatia ili kusudi pasiendelee kuwepo kwa marejeo ya mambo yaliyotokea katika mwaka huu ambapo palikuwa na kiangazi kirefu.
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya nyongeza. Kwa kuwa janga la mwaka huu na mwisho wa mwaka jana inalika nguvu za ziada za Serikali katika kutenga fedha za kutosha kuchimba mabwawa katika maeneo ya nyanda kame. Je, Serikali itaweka bayana idadi ya mabwawa yatakayoweza kujengwa ili kunusuru hali iliyotokea juzi isirejee kabla ya bajeti ya mwaka 2022/2023 kuanza?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba jambo hili la idadi hasa liwe ni jambo la utendaji kazi. Kwa hivyo, sisi tutawasiliana halmashauri yake tupate namba halisi ili tuweze kulifanyia kazi.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali ambayo yanatoa tumaini kwa vijana wa Jimbo la mikumi. Swali langu la kwanza; kwa kuwa Serikali itaangalia uwekezaji unaofaa katika bwawa hilo, je, mpango huo unahusisha pia uzalishaji wa vyakula vya samaki katika viwanda vidogo na vya kati katika eneo la Jimbo la Mikumi ili kukuza ufugaji wa samaki?

Mheshimiwa Spika, la pili, karibu na Zombo kuna reli ya mwendokasi ambako kuna mashimo makubwa ambayo walikuwa wanachimba kokoto wakati wa ujenzi huo. Mashimo haya makubwa yana potential ya kubadilishwa kuwa mabwawa kwa ajili ya ufugaji wa samaki lakini pia kwa ajili ya mifugo. Je, Serikali itakubaliana nami kwamba wakati umefika wa kuyatengeneza mabwawa haya ili kutatua tatizo letu? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Denis Lazaro Londo, Mbunge wa Jimbo la Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, umuhimu na uhitaji wa vyakula vya mifugo nchini hususan samaki ni mkubwa sana na kwa kadri tunavyoendelea kuhamasisha ufugaji wa samaki umuhimu umezidi kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Londo, kwamba tunahitaji uwekezaji zaidi. Katika Mkakati tulio nao ndani ya Serikali ni kuvutia uwekezaji wa uzalishaji wa chakula cha samaki.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mabwawa ama mashimo yaliyotokana na ujenzi wa reli ya SGR, nakubaliana naye na ni wazo jema sana.

Mheshimiwa Spika, sisi katika Wizara tumeanza mazungumzo na wenzetu wa reli ili kuhakikisha kwamba mabwaya yale tunayaongezea thamani kwa kuyatengenezea miundombinu ili yaweze kutumika kwa ajili ya shughuli za ufugaji pamoja na shughuli za ufugaji wa samaki. Ahsante sana.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Serikali inatambua ufugaji wa samaki kwenye mabwawa kule ukanda wa Ziwa Victoria na maeneo yote yanayozunguka na hasa maeneo ya kandokando kwenye miji mikubwa, zoezi la ufugaji wa samaki kwenye vizimba linaendelea kukua kwa kasi na tunaamini linaweza likatoa ajira nyingi sana kwa vijana.

Je, ni upi sasa mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba vijana wengi zaidi wanaingizwa katika shughuli hizi na kupewa fedha ili waweze kuwekeza kwenye ufugaji wa vizimba?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Mabula, Mbunge wa Nyamagana, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mkakati wetu ndani ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ni kwamba tumeweka hela kiasi cha shilingi milioni 154. Pesa hizi ni kwa ajili ya kwenda kufanya mpango wa matumizi bora, kwa lugha nyepesi, katika eneo la Ziwa Victoria, Mkoa wa Mwanza na Mkoa wa Kagera. Tunakwenda kufanya demarcation na pesa hii tumeipeleka katika Taasisi yetu ya Utafiti ya TAFIRI kwa lengo la kutuandalia maeneo mahsusi ambayo vijana watakwenda kuyatumia kwa ajili ya ufugaji wa vizimba.

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi, vijana hawa tutawaweka katika ushirika ambao utawasaidia kuweza kupata mikopo na kuweza kujifanyia shughuli zao.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali Wilaya ya Bunda inaishi karibu sana na Ziwa Victoria na Jimbo la Bunda ni kilometa 45 kutoka Ziwa Victoria. Sasa kwa sababu kuna pressure kubwa ya uvuvi wa samaki na kwa sababu sasa tunataka kupunguza hiyo pressure ya wavuvi wa samaki.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuweka mikakati ya kuweka vizimba katika Jimbo la Bunda na hasa pale kwenye mabwawa ya kuchimbwa kwa ajili ya kufuga samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni mkakati endelevu tulionao wa kuhakikisha kwamba tunakwenda kwenye eneo hili la ufugaji wa samaki na hasa upande wa Ziwa Victoria ambako kuna ufugaji wa kutumia vizimba na hivyo Jimbo la Bunda nalo litafikiwa.
MHE. JAFARY W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa shughuli hii ya ufugaji wa samaki inafanyika pia katika Jimbo la Rorya, kwa maana ya wilaya nzima, hasa ukizingatia kwamba umbali wa kutoka ziwa kuelekea kwenye maeneo ya wananchi haizidi hata mita tano. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia vijana wa maeneo yale ambao wanaishi karibu na ziwa ili kufanya na kuanzisha ufugaji huu wa samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chege, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeeleza, kwamba ufugaji wa samaki, hasa kwenye vizimba, upande wa Ziwa Victoria ndicho kipaumbele chetu cha kule tunakolekea ili kupunguza pressure ya uvuvi ule wa asili. Ili kuweza kufanikiwa katika lengo hili tunahamasisha uundaji wa vikundi, hasa vikundi vya Ushirika, hivyo namwomba Mheshimiwa Chege na Waheshimiwa Wabunge wengine wote wa eneo hili waweze kuwahamasisha vijana wale wajiunge katika vikundi ili tuweze kupata mikopo kupitia Benki yetu ya Kilimo na hatimaye kuweza kuifanya shughuli hii ambayo itawaingizia kipato na kukuza pato la Taifa letu.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Shirika la Umoja wa Mataifa la Kilimo na Chakula (FAO) limetangaza mpango maalum wa ufugaji wa samaki katika maneo mbalimbali duniani ikiwemo Ziwa Tanganyika. Je, Serikali yetu imechukua hatua gani za haraka za kushirikiana na shirika hili katika kufanikisha mpango huo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. FAO ni wadau wetu wakubwa na tunashirikiana nao kama Serikali. Hata hivyo, kwa jambo hili mahsusi alilolisema Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda ninaomba nimkaribishe kula swali mahsusi ili tuweze kulifanyia kazi. Ahsante.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza. Pamoja na nia njema ya Serikali kutaka kujenga mialo kwenye Forodha ya Nankanga na Ilanga, lakini kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu ndani ya Ziwa Rukwa kati ya Hifadhi ya Uwanda Game Reserve na ile Rukwa Lukwati.

Je, Serikali mna mpango gani wa kuweka alama za kudumu zitakazowafanya wavuvi wafanye shughuli zao za uvuvi bila kubughudhiwa na askari wa wanyamapori wa Uwanda Game Reserve pamoja na wale wa Rukwa Lukwati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili: Ziwa Rukwa ni moja kati ya maziwa ambayo yana mamba wengi hapa Tanzania na imesababisha wavuvi wengi kupoteza maisha. Nataka kujua, ili kuwalinda wavuvi wetu ndani ya Ziwa Rukwa, Serikali mmejipangaje kuleta vyombo vya uokozi ndani ya Ziwa Rukwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Deus Sangu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza anataka mpango wetu juu ya kuweka maboya. Hili tutashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Maliasili na Utalii ambayo ndiyo inasimamia hizi game reserves kwa ajili ya kuweza kuona namna tunavyoweza kutekeleza jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, halikadhalika, lile la mamba wanaokula wavuvi; kwa kuwa mamba pia ni rasilimali na inasimamiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii, naomba nirejee tena katika jibu la mwanzo kwamba tutashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Maliasili na Utalii na tutafanya mkutano wa pamoja ili tuweze kutafuta suluhu ya jambo hili, ikiwemo kupata vifaa vitakavyowawezesha wavuvi hawa kuweza kuokolewa. Ahsante sana.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja tu la nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mpaka sasa Halmashauri ya Mkalama ndio wanaotunza shamba hili; na kwa kuwa, hatuna ugomvi na Wizara na tunajali sana maslahi ya umma: Je, Wizara ipo tayari sasa kukaa meza moja na Halmashauri ya Mkalama ili tuweze kukaa na kujadili matumizi bora zaidi ya eneo hili kuliko kuendelea kuwa shambapori kama ambavyo lilivyo sasa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Isack Francis Mtinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, milango ya Wizara iko wazi. Tunawakaribisha viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, wakiongozwa na Mheshimiwa Mbunge makini, waweze kuja tukae mezani kuzungumza na kuona hatima njema ya eneo lile na hususan katika kuboresha mifugo yetu na huduma nyingine. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Katika Wilaya ya Mpwapwa kuna idadi kubwa sana ya mifugo, lakini changamoto yetu kule ni ukosefu wa mfumo rasmi wa upatikanaji wa madawa kwa ajili ya kutibu mifugo yetu. Wafugaji kule wanategemea sana walanguzi ambao wakati mwingine wamewauzia dawa feki na zimewasababishia hasara. Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu rasmi wa kuhakikisha kwamba wafugaji wetu wanapata dawa za kutibu magonjwa ya mifugo katika maeneo yao?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Malima, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Wizara ya Afya kwenye vitengo vyetu vya Baraza la Veterinary Tanzania na TMDA kwa pamoja tunafanya operations za mara kwa mara za kufuatilia dawa zisizo na viwango. Kwa mwaka jana tulikamata na hatua za kisheria zilichukuliwa na mwaka huu pia vile vile Mkoani Mwanza tayari yuko mzalishaji na msambazaji wa dawa feki ambaye tumemkamata.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wetu sasa kupitia Baraza hili ni kuhakikisha kwamba udhibiti wa dawa hizi unaimarishwa ikiwa ni pamoja na kuzalisha dawa nyingi zaidi zilizobora kupitia viwanda vyetu vya hapa nchini pamoja na kiwanda cha Serikali kilichoko pale Kibaha kwa maana cha TVI ili wafugaji wetu waweze kupata uhakika wa chanjo na dawa zenye kukidhi viwango.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mwani limekuwa ni zao ambalo linaingizia nchi nyingi fedha za kigeni na uzalishaji Tanzania kwa sasa ni tani 3,500 tu, lakini uhitaji uliopo kwa wanaotu-approach nchini kwetu ni tani zisizopungua 10,000. Swali langu ni kwamba ni upi mkakati wa Serikali wa kuongeza uzalishaji wa mwani nchini? Hilo ni swali la kwanza.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kutoka Tanga, ukanda huu wa mwambao wa bahari ya Hindi mpaka Mtwara, zaidi ya kilometa 1,084 kuna vikundi vya wanawake visivyopungua 8,000. Naomba kujua ni nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha masoko kwa wanawake hawa wanaozalisha mwani nchini na bei yenye tija?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa, Engineer Mwanaisha Ng’azi Ulunge, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, la kwanza katika jibu la msingi nimeeleza juu ya mkakati wa Serikali wa kuweka shilingi bilioni 3.3 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakopesha vikundi vya akina mama kamba na kitu tunaita taitai, na kitu tunaita mbegu ili waweze kuongeza uzalishaji. Na hiyo tutagawa katika vikundi vyote pamoja na hivi vikundi alivyovitaja Mheshimiwa Ulenge. Kwa hiyo, hilo litasababisha kuongezeka kwa uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, suala la bei na soko, nataka niwahakikishie kwamba kwa hali ilivyo na kwa uelekeo tunaouona, soko la mwani linazidi kukua siku hata siku na kwa msingi huo, tutakapokuwa na uzalishaji mkubwa, sasa uwezo wa kuweza kuliongoza soko katika bei utakuwa ni mkubwa, ni pamoja na kuweka mkakati wa bei elekezi ili zisishuke.

Mheshimiwa Spika, kama mwani aina ya spinosio uuzwe 800 kwenda juu, kama mwani wa aina ya kotonii uuzwe 2,000 kwenda juu. Huo ndiyo mkakati wetu tunaouelekea. Nashukuru.
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Mkandarasi huyu alipewa kazi hii toka mwaka jana Mei, 2021 na kazi yenye ilikuwa ni sehemu ya kutengeneza mwalo wa kupokelea samaki pamoja na vipimo vya samaki, hauoni sasa muda tayari umeshafika zaidi ya mwaka mmoja na miezi minne, ni lini sasa kazi hiyo ya ujenzi wa banda hilo utakamilika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la nyongeza ni kwamba, Mheshimiwa Naibu Waziri alifika katika eneo hilo la mradi na pamoja na kutembelea eneo hilo alikwenda pia kuangalia mabwawa ya kunyweshea mifugo katika Jimbo la Sengerema, lakini mpaka leo hii mabwawa hayo hayajapata fedha. Je, ni lini fedha zitaletwa kwa ajili ya kuyaziba mabwawa tisa yaliyopasuka katika Jimbo la Sengerema?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Tabasamu, Mbunge wa Sengerema, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa kukamilisha unafanyika kwa haraka mara baada ya kuvunja mkataba, hivi sasa wataalam wetu wapo kazini kuhakikisha kwamba kazi ile ya wananchi inakamilika ili waweze kupata huduma wanayostahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili anataka kujua juu ya mabwawa yake lini yatapata fedha. Tayari kwa utaratibu wa Sheria ya Manunuzi tumekwishatangaza tenda na tupo katika hatua ya kupata wakandarasi na hatimaye yale yaliyopangiwa kwenye jimbo lake yatapata fedha na wakandarasi watatekeleza kazi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimshukuru Mheshimiwa Tabasabu kwa ushirikiano mkubwa anaotupatia, ahsante sana.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Hapa siku za karibuni tumesikia taarifa kupitia vyombo vya habari kwamba uhifadhi wa samaki hapa nchini kwenye baadhi ya maeneo, samaki wanahifadhiwa kwa kutumia dawa za kuhifadhia maiti, jambo ambalo linaleta taharuki kwa wananchi na wananchi hawajui nini cha kufanya ili wasipate hao samaki waliohifadhiwa kwa namna hiyo.

Je, ni nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha samaki hao hawahifadhiwi kwa vitu hivyo ambavyo vinasababisha kansa kwa Watanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili alilolisema Mheshimiwa Paresso ni hypothesis halina hakika hadi sasa hivi. Ni kwamba watu wanahisia kuwa kiko kitu cha namna hiyo na ndiyo maana Mheshimiwa Makamu wa Rais alipokuwa Jijini Mwanza aliagiza Wizara ya Afya ifanye utafiti ili kama ni kweli kinafanyika kitu cha namna hiyo basi kizuiwe mara moja. Naomba niwatoe hofu Watanzania hakuna jambo linalohusu tuchukue samaki kutoka Mwanza tulete Dodoma au tupeleke Dar es Salaam kwa kuhifadhi na maji ya maiti, halipo jambo la namna hiyo! Naomba wawe na uhakika ya kwamba samaki wanaovuliwa na wavuvi wetu na wanaokwenda katika masoko mbalimbali wako salama hawana shaka yoyote. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana Mheshimiwa kwa majibu mazuri, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, moja, ni lini Serikali itapeleka maji katika Kata za Mtambula, Luhunga na Mninga kule Mufindi Kusini?

Mheshimiwa Spika, pili, ni lini Serikali itakamilisha miradi ya maji ya Malangali, Nambalamaziwa na Igohole ambayo tayari Serikali imeshaanza kutenga fedha?
NAIBU WAZIRI MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kihenzile, Mbunge wa Mufindi Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, la kwanza, Serikali imejipanga hivi sasa katika kata zile tatu alizozitaja inafanya utafiti wa kupata vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, la pili, tayari taratibu za manunuzi zimekwisha kukamilika na mnano mwezi Desemba utekelezaji wa mradi utaanza.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Miradi mingi ya maji ikiwemo ya Jimbo la Ukerewe inasuasua kukamilika kwa sababu ya mchakato mrefu wa kupata msamaha wa kodi. Nini mkakati wa Serikali kupunguza urasimu kwenye kupata misamaha ya kodi ili miradi hii ya maji iweze kukamilika haraka? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli na hivi sasa Serikali inaendelea na jitihada, Wizara ya Maji kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha kufanya utaratibu wa kuhakikisha kwamba misamaha yote ya kodi inayohusu sekta ya maji iweze kupitiwa na kupatikana suluhu mapema ili kuweza kuwanufaisha wananchi.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi, mkakati wa kutoa maji Ziwa Tanganyika ni mkakati wa muda mrefu. Nataka kujua mkakati wa muda mfupi wa kuwasaidia zile kata tano za Wilaya ya Nkasi, Kata ya Namanyele, Nkomoro, Majengo pamoja na Isunta kuepusha hiki kipindi ambacho wanakipitia kigumu?
NAIBU WAZIRI MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jumla ya fedha shilingi bilioni 657 zimetengwa na iko miradi 381 mipya. Ninayo imani kwamba katika hii miradi 381, miradi hii ya Nkasi ni miongoni mwao. Kwa hiyo, Mheshimiwa Aida uendelee kufuatilia katika kuhakikisha kuwa wananchi wa Nkasi na wenyewe wanapata faida hii ya maji safi na salama.
MHE. YAHYA ABDULWAKIL AHMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri na ya kutia moyo katika ununuzi wa meli hii, naipongeza Serikali kidogo, nina swali moja la nyongeza.

Kwa vile ununuzi wa meli hizi utashirikisha Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, watafaidika wa meli mbili na mbili itafaidika Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo Tanzania Bara, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshirikishwa katika hatua hizi za awali za manunuzi haya? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ushirikishwaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar upo wa kiwango kikubwa kabisa na jambo hili linaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu ikishirikiana na Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais upande wa Zanzibar na Wizara zetu pia vilevile ya Mifugo na Uvuvi na Wizara ya Uchumi wa Bluu lakini na Mashirika yetu vilevile ya TAFCO na ZAFCO yote yanafanya kazi hii kwa pamoja. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Abdulwakil kwamba Serikali inashirikishwa ipasavyo. Ahsante.
MHE. SALMA RASHID KIKWETE: Mheshimiwa Spika ahsante sana. Naipongeza Serikali kwa mpango kabambe wa ununuzi wa hizo meli nane na wataanzia na meli nne. Je, Serikali ina mpango gani kwa mikoa yetu miwili Mikoa ya Mtwara na Lindi juu ya upatikanaji wa meli hizi angalau moja ukizingatia kwamba kule kuna samaki wengi. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Kikwete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba meli hizi kwanza zitamilikiwa na Shirika letu la TAFCO kwa ubia na mashirika binafsi na kwa upande wa Mikoa ya Lindi na Mtwara na kwingine kote ambako shughuli za uvuvi zinafanyika, Serikali imekuja na mpango madhubuti wa kukopesha wavuvi ambapo boti zaidi ya 150 zitakopeshwa nchi nzima katika maeneo ambayo shughuli za uvuvi zinafanyika na tayari maelekezo na maombi mbalimbali tumekwishayapokea ili harakati na utaratibu wa kuweza kuwapata wenye sifa za kukopa mikopo hii zifanyike na hatimaye waweze kupata mikopo isiyokuwa na riba.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha, ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kimsingi ninachotaka kufahamu ni kwamba mradi huu utakamilika lini? Kwa sababu kumekuwa na tatizo kubwa sana la maji kwenye Wilaya ya Newala, Tandahimba pamoja na Nanyamba hasa zaidi wakati wa kiangazi ambacho ndiyo tunakwenda sasa hivi. Sasa nataka kufahamu ili kuwapa comfort wananchi, mradi huu utakamilika lini ili waweze kupata maji safi, salama na ya kutosha?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecil Mwambe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika jibu la msingi, nimeeleza kuwa awamu ya tatu na ya nne itakamilika mnamo mwezi Desemba, mwaka huu wa 2022.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kufuatia ujenzi wa Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko, wananchi wa Kilwa Masoko tumeandaa eneo la kutosha kwa ajili ya sekta mbalimbali. Je, Serikali sasa iko tayari kuhakikisha kwamba sekta rafiki au taasisi rafiki na bandari ya uvuvi kama vile Chuo cha Uvuvi, viwanda vya kuchakata samaki pamoja na soko la samaki vinajengwa Kilwa Masoko?

Swali la pili, wapo wananchi wapiga kura wangu ambao wamefanyiwa tathmini ili kupisha ujenzi wa Bandari ya Uvuvi wakiwemo Ndugu Mwanawetu Zarafi, Ndugu Fatima Mjaka, Ndugu Fadhila Sudi pamoja na Ndugu Suleiman Bungara (Bwege) na wenzao 50.

Je, ni lini Serikali itakwenda kulipa fidia kwa wapiga kura wangu hawa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza naomba nimhakikishie kuwa ujenzi wa bandari hii kubwa ya mfano na ya kielelezo katika Taifa letu inaendana na yote aliyoyasema ya uwepo wa miundombinu wezeshi. Kwa hivyo, nataka nikuhakikishie ya kwamba Serikali ya Awamu ya Sita imeliona jambo hili na nikipaumbele chake. Kutakuwepo na soko, patakuwepo na maghala ya kuhifadhia bidhaa za chakula, kutakuwepo na miundombinu mingine yote inayoendana na hadhi ya bandari ya uvuvi ya kisasa na ya Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ni hili la tathmini naomba nilichukue jambo hili kwa kuwa jambo hili tunashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi kwa maana ya Mamlaka yetu ya Bandari (TPA), kwa hiyo nataka niwahakikishe nalichukua hili jambo nakwenda kulisimamia kuhakikisha kwamba wananchi hawa waweze kupata haki yao.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itakuja na mpango wa ujenzi wa vizimba vya kufugia samaki katika Ziwa Duluti kwa lengo la kupunguza tatizo la ajira kwa vijana kule Arumeru Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Pallangyo, Mbunge wa Arumeru, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan ilitenga kiasi cha Shilingi Bilioni 20 kwa ajili ya kuanza mradi maalum wa vizimba vya Samaki. Vilevile tunao mradi kwa ajili ya maeneo ya ufugaji samaki nje ya vizimba kwa maana ya mabwawa. Naomba niseme tu kuwa Ziwa Duluti tutalifanyia tathmini ikiwa kama ni katika maeneo yenye kuweza kufanyiwa shughuli hizi za vizimba katika mwaka mwingine wa fedha tutaliwekea mpango na lenyewe, kwa sababu siyo kila mahali tunaweza kujenga vizimba kulingana na taarifa za kitaalam. Ahsante. (Makofi)
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, naomba niwe na maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza: Kwa kuwa nyavu nyingi zinaagizwa kutoka nje ya nchi na kuingizwa ndani ya nchi, lakini mwisho wa siku, mvuvi ndio amekuwa mhanga mkubwa wa hizi nyavu: Je, Serikali imewahi kuwawajibisha watendaji wengine kama ilivyowataja kwenye swali la msingi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha wavuvi kupata vifaa vya kisasa ili waondokane na zana za uvuvi zilizopitwa na wakati?

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Eng. Stella Simon Fiyao, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali kuhusu je, wapo ambao wamewahi kuwajibishwa kutokana na kwamba nyavu hizi huwa zinaagizwa kutoka nje au zinazalishwa na watu, wapo? Zipo kesi kadhaa ambazo zimewahusisha waagizaji na zilizowahusisha watengenezaji na kesi hizi zote tulipokwenda Mahakamani Serikali ilifaulu kwa kushinda kesi zile. Zipo kesi nyingine ambazo hata sasa bado zinaendelea. Wako watendaji ambao walichukuliwa hatua mbalimbali na wengine kesi zao bado ziko Mahakamani.

Mheshimiwa Spika, swali la pili alitaka kujua juu ya uwezeshaji wa makundi ya wavuvi kwa kupata vifaa vya kisasa. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na Serikali yetu ya Awamu ya Sita. Tunayo program kubwa ambayo inaendelea hivi sasa ya kuhakikisha kwamba tunakwenda kukopesha boti za kisasa takribani 150 hadi 160 kwa wavuvi wote nchini, wale watakaokidhi vigezo. Boti hizi zitakuwa na vifaa kama vile fish finder kwa maana ya kile kifaa cha kujua Samaki walipo, vilevile eneo la kuhifadhia samaki takribani tani moja hadi tani moja na nusu, GPS na zitakuwa zimeunganishwa katika Satelite ili mvuvi kabla hajatoka kwenda katika uvuvi awe tayari na picha ya kujua mahali walipo samaki. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu haya ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi bilioni mbili aliyoisema kwenye majibu yake ya msingi, ni ndogo sana kutokana na swali lilivyoulizwa wa kila Kijiji kuchimbwa mabwawa.

Je, Serikali ina mpango gani sasa kuongeza bajeti ili maeneo haya anayoyasema yaweze kuchimbwa mabwawa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; tumeleta maombi ya Mbulu Vijijini kuchimbiwa mabwana katika vijiji vya Gidihim, Eshkesh, Yaeda, Masieda na Endagichan na wewe Naibu Waziri unafahamu: Lini mtatuchimbia hayo mabwawa kama tulivyoomba?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Flatei Massay. La kwanza ni juu ya kuongezwa kwa bajeti. Nimelipokea jambo hili na kwa kuwa sasa ndo tuko kwenye Bunge la Bajeti, namwomba Mheshimiwa Flatei Massay na Waheshimiwa Wabunge wengine, tusiwahishe shughuli; tusubiri, nina imani mambo mazuri yanakuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni hivi vijiji vyake alivyovitaja. Naomba mimi na yeye tuzungumze mara baada ya hapa kuona namna ambavyo tunaweza kujipanga kwa ajili ya kutekeleza kile alichokiomba. Ahsante. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii. Serikali iliwaahidi wananchi wa Kijiji cha Kivingo Kata ya Lunguza ambao wako pembezoni mwa hifadhi ya Taifa Mkomazi, kuwajengea bwawa kwa ajili ya shughuli za kilimo na lambo kwa ajili ya shughuli za ufugaji; na Mamlaka ya Hifadhi Tanzania (TANAPA) ilikuwa imeanza huo mchakato. Sasa ni lini Serikali itahakikisha kwamba bwawa hili linachimbwa na lambo kwa ajili ya mifugo linapatikana?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali zuri la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo juu ya ahadi iliyotolewa na Shirika letu la TANAPA kuhusu kujenga lambo katika Kijiji cha Kizingo pembeni ya hifadhi ya Taifa ya Mkomazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali tunafanya kazi kwa pamoja na TANAPA ni chombo chetu, naomba nimwahidi Mheshimiwa Mbunge ya kwamba nitazungumza na Mheshimiwa Waziri wa Maliasiri na Utalii tuwakumbushe TANAPA tuweze kuifanya kazi hii ya wananchi. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Naishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Miezi michache iliyopita Waziri wake alifika kwenye Jimbo langu akaangalia hatari kubwa ya lambo la Salamakati ambalo bado kidogo sana kutoweka. Kutokana na mvua zilizonyesha, lambo lile lina hatari kubwa sana ya kubomoka lote. Mheshimiwa Waziri aliahidi kuweka mikakati ya dharura ya kuziba lile lambo kabla halijabomoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupata majibu kuna mikakati gani ya kuziba lambo la Salama ambalo liko hatarini kubomoka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Naibu Waziri anaweza kunieleza nini kuhusu namna gani anaweza kwenda kuziba hilo lambo au kulijenga upya au kuliziba ile nyufa inayotaka kubomoka?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza tumepokea shukrani kutoka kwa Mheshimiwa Boniphace Getere. Pili ni juu ya ukarabati wa hili lambo. Naomba nilichukue jambo hili na kwenda kulisukuma ili liweze kufanyika sawa na ahadi ya Mheshimiwa Waziri.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Bwawa la Mtera lililoko Halmashauri ya Iringa Vijijini kumekuwa na upungufu mkubwa wa Samaki na hivyo kuathiri biashara ya samaki katika Nyanda za Juu Kusini na masoko mengine.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kujenga mashamba darasa ya samaki hasa Jimbo la Kalenga ili sasa tuweze kufundisha vijana wengi kufuga samaki na hivyo kufufua uchumi wa vijana kwa namna hiyo? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Kalenga, juu ya mashamba darasa ya kufugia samaki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo program ambayo itakwenda katika baadhi ya Halmashauri zetu na yawezekana kabisa moja ya Halmashauri itakayofaidika na program hii ya mashamba darasa ya samaki ikawa ni Halmashauri ya Kalenga.

Kwa hiyo, naomba nilichukue jambo hili la Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kulifanyia kazi na wananchi wa Kalenga waweze kufaidika. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi. Serikali iliahidi Bwawa la Mhanga katika Halmashauri ya Itigi na wakaanza ujenzi, lakini ukasimama: Je, Waziri yuko tayari kwenda nami kuona utekelezaji wa ahadi hii nzuri ya Serikali ili wananchi wawaone aweze kusukuma malizio lile lambo ambalo linajengwa pale Muhanga?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishe kaka yangu Mheshimiwa Massare, niko tayari kwenda Itigi. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa majibu ya Waziri yanakiri kwamba ushuru mkubwa ulilenga kulinda viwanda vya ndani na ni asilimia 80 ya thamani ya mzigo ukiwa bandarini, sasa kuna ushahidi ulio dhahiri kwamba viwanda vya ndani vilivyokuwa vikilindwa vingi vimekufa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna kiwanda cha Himo ambacho na chenyewe kiko hai, lakini ngozi inayohitajika ni ya kilogram 12 ambayo inapatikana Bukoba. Sasa swali langu kwa Serikali, wafanyabiashara wa ngozi wamekwama ushuru mkubwa, viwanda vya ndani vimekufa, Serikali haipati mapato ya kutosha. Sasa, je, kwa kuzingatia kwamba hata Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki linapokuja suala la masilahi ya ndani na yenyewe wala haitekelezi makubaliano yenu, kwa nini Serikali isifanye tathmini upya, kuangalia uamuzi wake ili kulinda wafanyabiashara wa ndani wa Ngozi na kulinda nchi? Hilo swali langu la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tunaingia mwaka mpya wa fedha, tunaamini Wizara ya Mifugo chini ya Mawaziri akiwemo kijana makini, hivi bado hawajafikiria mwaka huu wa kikodi kuangalia hili eneo muhimu? Kwa sababu ni dhahiri shahiri kuna ngozi zinaoza huko mtaani kwa maelfu, hawajaangalia hili eneo ili wasaidie nchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa
Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Halima James Mdee, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni juu ya tathmini Serikali kutazama kulingana na hali halisi ya biashara ya Ngozi. Nimelipokea jambo lake hili la kusema tufanye tathmini ni jambo jema.

Vilevile nimshukuru amekiri na ndio ukweli wenyewe kwamba tumeweka viwango hivi vya kikodi ndani ya Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki kwa lengo la kulinda viwanda vyetu vya ndani. Hii 80 percent tuliyoiweka imewekwa makusudi kwa ajili ya ku-discarage kutoa ngozi ikiwa ghafi kwenda nje ya mipaka ya Taifa letu ili kulinda ajira na kupata kipato zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, niseme ukweli bado ngozi nyingi inakwenda nje ikiwa ghafi, pamoja na ushuru huo mkubwa inakwenda Nigeria, Ghana ambako huko wanaitumia kama chakula, kwa hiyo hili lifahamike. Hii ngozi tunayosema kwamba iko vijijini inaharibika, inawezekana lakini kwa uhitaji wa ngozi wa sasa jambo la ngozi kuharibika ni kiasi kidogo sana, yawezekana wahitaji wanaohitaji hizi ngozi hawajaweza kuvifikia vile vijiji ambavyo vina hiyo ngozi inayoharibika. Hata hivyo, niseme tu kwamba tutaimarisha sasa mfumo wetu ili hata ile iliyoko kule vijijini iweze kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, amezungumza juu ya maboresho ya kikodi. Hili jambo pia vilevile nimelichukua, kwa ajili ya kuweza kuangalia maslahi mapana ya sekta hii ya ngozi.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza na nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa wanawake wengi ndiyo wanajishughulisha na ukaushaji wa dagaa, je, Serikali ina mpango gani maalum wa kuwasaidia kwa haraka wanawake hawa ili kupata tija zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Maryam Mwinyi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango maalum tulionao, la kwanza Serikali imejikita katika kulitangaza zao la dagaa kuwa ni zao la kimkakati na lengo na dhamira ya Serikali ni kulipa thamani zao hili kulifungulia masoko na kuweza kuwahakikisha hata mabenki yaweze kuwa na utayari wa kuwakopesha akinamama wanaojishughulisha na shughuli hizi za ukaushaji wa dakaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni kufungua masoko ya duniani na hivi tunavyozungumza zao la dagaa limekuwa na thamani kubwa sana katika soko la dunia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo pia kama nilivyosema katika jibu la msingi ni kuwawezesha kupata mikopo kupitia Benki yetu ya kilimo na kuhimiza halmashauri zetu kupitia ile asilimia nne ya akinamama, kuwasaidia na kuwakopesha zaidi akinamama wazalishaji hasa kundi hili la wavuvi linalokausha dagaa na kufanya biashara hii ya dagaa. Ahsante.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Kwa kuwa dagaa ni shughuli ambayo wanawake wanajishughulisha nayo sana na shughuli hii inaendana sambamba na suala zima la mwani. Je, Serikali ina mpango gani kuhusiana na suala la mwani kuwasaidia wanamwani hawa kutupatia vifaa? Sambamba na vifaa kutupatia au kututafutia soko la mwani kwa ajili ya ustawi wa wanawake?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Kikwete, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wetu katika mwani, kwenye bajeti yetu ya mwaka huu wa fedha 2022/2023, tumetenga takribani Shilingi Bilioni 3.4 kwa ajili ya kununua vifaa kwa maana ya kamba, taitai na mbegu kwa ajili ya kuzitawanya katika vikundi vya akinamama mwambao wote wa pwani kuanzia Mkinga mpaka kule Moa Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile mkakati wetu ni kujenga maghala, nia ni madhumuni ni kuongeza uzalishaji. Hivi sasa tunazalisha tani 3,500 tunataka tufike tani 10,000 hadi 15,000 ili sasa tuwe na kauli katika soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nimhakikishie Mheshimwia Salma Kikwete lakini na Wabunge wote kwamba, Serikali tumejipanga vema, tunalo lengo hata la kuingiza mwani katika mtindo wa stakabadhi ghalani ili tuweze ku-control bei ambayo kwa muda mrefu sana imeonekana ni yenye kuyumba. Ahsante sana.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Serikali katika bajeti yake ya mwaka 2021/2022 ilituahidi vichanja kwa wavuvi wa dagaa; na kwa kuwa hata kwenye bajeti yake ya 2022/2023, bado ametuahidi vichanja na Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kuna vichanja 80 watapeleka. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka vichanja hivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swal la nyongeza la Mheshimiwa Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kabisa mwaka huu niliousema wa fedha wa 2023/2024, baada ya kuwa tumekamilisha taratibu zote za kitaalam, ambazo ndiyo zilizokuwa zikitukwamisha tutakwenda kutekeleza ahadi hii ya Serikali kwa hakika kabisa.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nami naipongeza Serikali kwa kuja na mradi mzuri huu wa kuinua wavuvi na kwa kuwa Wilaya za Mkuranga na Kibiti ni wilaya ambazo zinajihusisha na uvuvi sana na kundi kubwa la wanawake wanafanya shughuli hii. Je, ni lini mradi huu wa kuinua wavuvi utawafiki wananchi wa wilaya hizi mbili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalum, Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Mkuranga na Kibiti ni miongoni mwa wilaya zitakazofaidika na program hii, lakini vilevile zitafaidika na program kubwa inayokwenda kwa jina la Tanzania Scaling up Blue Economy ambapo tutajenga maghala ya kuhifadhia samaki, masoko vikiwemo na hivi vichanja. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Alice na Wabunge wengine wa Mkoa wa Pwani, Tanga, Lindi na Mtwara pamoja na wengine wote kwamba tumejipanga vema na hili tunakwenda kutekeleza.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kabisa niipongeze Serikali kwa kutuletea pesa katika miradi hiyo aliyoitaja, Mradi wa Chala, Kate, Mtuchi, Kandasi na sehemu zingine zote. Hata hivyo miradi hiyo ni kama imetelekezwa. Wananchi wanalalamika hakuna kwa kupeleka ng’ombe kwenda kuogelea. Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itaweka mkakati madhubuti wa kusimamia miradi hii iweze kutekelezeka?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Wilaya ya Sumbawanga DC ina mifugo mingi. Je, ni lini Serikali itajenga mabwawa ya kutosha kwa ajili ya mifugo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ni mkakati gani wa Serikali juu ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na umadhubuti kwenye usimamizi wa miradi hii? Tumejaribu kuona namna wa kurekebisha mfumo wetu na mfumo ambao tutakwenda nao katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 ni wa kupeleka fedha hizi moja kwa moja kwenye maeneo ya wanufaika, kwenye vijiji ili waweze kusimamia miradi hii ambayo itakwenda kuwanufaisha wananchi wao wenyewe moja kwa moja. Ambapo kwa sasa tunatumia mbinu ya kwamba miradi inalipwa na Wizara ingawa inasimamiwa na Halmashauri za Wilaya. Kwa hiyo tunaamini kwamba baada ya kuboresha mfumo huu sasa hakutakuwa na uzubaifu tena wa miradi yetu.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ni lini tutapeleka miradi mipya ya mabwawa kwa kuwa kuna ng’ombe wengi kule Nkasi? Naomba Mheshimiwa Bupe atupatie haya maeneo ili tuangalie katika bajeti hii ya mwaka huu kama tunaweza pia kupeleka miradi hii katika Jimbo la kule Nkasi.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Jimbo la Kalenga tulileta maombi matatu ya kujenga majosho katika Kata ya Kiwele, Mgela, Saadani pale Masaka pamoja na Ifunda Udumuka.

Je, ni lini Serikali sasa itatuletea fedha hizo ili tujenge hayo majosho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Kalenga, anayetaka kufahamu ni lini Serikali itakamilisha miradi ya majosho katika vijiji alivyovitaja kwenye Jimbo la Kalenga.

Mheshimiwa Spika, tumeshapeleka jumla ya fedha, shilingi bilioni 5.4 katika Halmashauri 80 na tumebakiza kiasi kidogo cha takribani shilingi milioni 500 ambapo tunataka twende kukamilisha hivi sasa. Mheshimiwa Kiswaga nitaomba baada ya Bunge unipatie hivyo vijiji ili nitazame kuona kwamba kama ni katika vile vilivyosalia na hatimaye viweze kupata fedha na miradi ile iweze kukamilika.
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Wizara ya Mifugo ikiongozwa na Waziri na wewe Mheshimiwa Naibu Waziri, mlikuja wakati wa janga la mwaka 2020 la ukame Wilayani Simanjiro na kushuhudia vifo vya mifugo mingi, mliahidi kutokana na upungufu wa majosho tuliokuwa nayo mtatujengea au mtatoa fedha ya majosho 20; kinyume chake, bajeti iliyofuata mwaka 2021 mmetupa majosho mawili.

Je, lini sasa Serikali itatoa hizo shilingi milioni 400 ili kukamilisha majosho yale ambayo yataungana na nguvu za wananchi ili kuepusha vifo vya mifugo katika nyanda hizo kame?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ole-Sendeka Mbunge wa Simanjiro, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika maeneo ambayo yamekuwa yakiathirika kwa kiasi kikubwa na ukame ni pamoja na Mkoa wa Manyara hasa Wilaya ya Simanjiro na Wilaya ya Kiteto. Katika bajeti ya mwaka huu, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa majosho na mabwawa.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Ole- sendeka atupatie vile vijiji ambavyo wamekubaliana viende vikajengewe majosho ili kusudi Serikali iweze kutekeleza kazi hii ya kuhudumia wafugaji, ahsante.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; tatizo la majosho lipo pia katika Jimbo la Geita Mjini na majosho yaliyopo yanashindwa kufanya kazi kwa sababu hayana maji.

Je, Wizara ina mkakati gani wa pamoja kwamba pale ambapo kuna majosho panakuwa na maji ya uhakika ili majosho yaweze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni mkakati gani wa Serikali wa kuhakikisha kuwa tunakuwa na maji ya uhakika katika yale maeneo? La kwanza, haya maeneo huteuliwa au huchaguliwa na wananchi wao wenyewe kwa maana ya kwamba tunakwenda kujenga josho kulingana na matakwa ya wananchi, kulingana na mazingira yao.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali imeendelea kujenga visima virefu na mabwawa katika baadhi ya maeneo. Kwa hiyo, kama lipo josho ambalo kwa hakika kabisa liko tatizo la maji kwenye eneo hilo, hususan katika Jimbo la Mheshimiwa Kanyasu alikotaja hapo Geita, tunaomba jina la kijiji hicho ili tutazame katika bajeti zetu ili wananchi wale waweze kupata huduma hiyo.

Mheshimiwa Spika, vile vile mkakati wetu wa Serikalini ni kuungamanisha huduma hizi za maji kati yetu Wizara ya Mifugo na wenzetu wa Wizara ya Maji ili kusudi pale penye maeneo ambayo huduma ya maji kwa ajili ya binadamu ipo, pia huduma hiyo iweze kwenda kuhudumia mifugo.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naishukuru Serikali kwa majibu mazuri: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, nchi yetu inauza ngozi ya bilioni 10 tu kwa mwaka, lakini nchi hii-hii ndiyo ambayo imebarikiwa kuwa na mifugo mingi zaidi.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kuongeza uzalishaji huo kwenye hivyo vituo viwili ambavyo vina-process mpaka mwisho ikiwepo Himo Tanneries na Moshi Leather Industries ili waweze kukidhi uhitaji wa nchi hii baada ya kufunguliwa kiwanda cha uzalishaji wa Kilimanjaro International Leather Industries?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Serikali ina mkakati gani kutoa elimu kwa wananchi wake ili kuhakikisha kwamba, mifugo inatoa ngozi bora na salama katika kipindi chote cha mwaka, ili kutoa ajira zaidi kwa vijana, wakiwemo vijana wa Kilimanjaro? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shally Raymond, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli lengo letu kama Serikali ni kuona uzalishaji kwenye viwanda vyetu vya ndani unaongezeka, jitihada kadhaa zinafanywa, ikiwemo kuondoa changamoto na kuboresha mazingira ya biashara. Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kushughulikia changamoto hizo ikiwa ni pamoja na ile ya kuondoa tozo na kodi mbalimbali zenye kuweka mkwamo wa upatikanaji wa malighafi na ushindani kwenye biashara. Baada ya kuyafanya haya tunayo imani kuwa, viwanda vyetu sasa vitapokea malighafi nyingi kutoka kwa wazalishaji ili kuviwezesha kufanyakazi yake kwa ufasaha zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili; ni mkakati gani juu ya elimu ni kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan imetenga fedha, mwaka huu tumetenga fedha kwa ajili ya kutoa elimu kwa wachunaji wa ngozi, lakini pia vilevile kununua vifaa kama computers, ili tuweze kuwa na record ya uzalishaji sahihi wa ngozi na hatimae kuwawezesha kuwaingiza katika masoko ikiwemo viwanda vyetu ambavyo vinazalisha hapa nchini, ambavyo tayari Mheshimiwa Shally Raymond ameshavitaja. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali. Kutokana na Takwimu za Serikali yenyewe, hali ya Ziwa Victoria hususani upatikanaji wa mazao ya samaki ni mbaya sana. Kulingana na viwango ambavyo tumejiwekea katika Ziwa lolote samaki wazazi wanapaswa kuwa kati ya asilimia 3-5 lakini kwa Takwimu ambazo zimetolewa na Serikali hii katika Ziwa Victoria samaki wazazi wako chini ya asilimia 0.85. Swali la kwanza; sasa naomba Serikali inipe majibu upungufu huo hausiani na uvuvi haramu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Task Force zimekuwa zikiendelea Ziwa Victoria, hawa ambao wanatumwa kwenda kufanya hiyo kazi ni wasomi, lakini hawana weledi wowote na masuala ya uvuvi. Matokeo yake wamekuwa wakikamata hizo zana haramu wanawapiga faini zisizo na Kanuni wala Sheria wala sijui nini, baada ya kuwapiga faini wanawarudishia zile zana haramu ambazo zinasadikiwa kuwa ni zana haramu.

Je, Serikali haioni kwamba inaendekeza huo uvuvi wa haramu kwa kutumia pesa ya walipakodi wa Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, upungufu hauhusiani na uvuvi haramu? Kwa namna yeyote ile upungufu wa samaki wazazi unahusiana na uvuvi haramu na ndiyo maana tumeweka mkakati shirikishi kama Serikali kupitia Vyombo vyetu vyote na sasa tunakwenda katika kutekeleza mkakati ule ambao utakwenda kunusuru na kulinda moja; samaki wazazi lakini mbili rasilimali nzima na kwa hivyo itapelekea kupatikana kwa uendelevu wa rasilimali hii muhimu kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, amehusianisha juu ya vitendo vya baadhi ya maafisa wetu wasiokuwa waaminifu na waadilifu. Nakiri yawezekana wako maafisa wanaofanya vitendo vya kinyume na maelekezo na maagizo ya Serikali. Tuko tayari kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge, ikiwa anafahamu watumishi wanaofanya hivyo, Taratibu, Sheria na Kanuni za Kiutumishi zipo, nataka nimuahidi yeye kwamba tutachukua hatua madhubuti kwa yeyote ambaye anashiriki katika kuharibu operations na shughuli za Kiserikali zenye lengo jema kabisa la kulinda rasilimali za nchi hii, ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwa kuwa Serikali ina mpango wa kutoa mikopo ya zana za kisasa za uvuvi kama boti pamoja na pesa kwa ajili ya kufanya uvuvi wa kuvua samaki kwa njia ya vizimba kama njia ya kuzuia uvuvi haramu. Je, ni lini sasa mikopo hii itawafikia wavuvi wetu? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joeseph Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejidhatiti katika kuondoa uduni na kero ya Wavuvi kutumia vyombo hafifu na kwa hivyo kupelekea kupatikana kwa vyombo vya kisasa sasa ni lini tunawapitia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari hatua za kimanunuzi zimekalika. Tunazo boti takribani 160 za kisasa zitakazogawiwa kwa wanufaika Wavuvi waliotimiza viwango ambavyo viliwekwa na Serikali na miongoni mwa Wavuvi hao wapo wa kule Ukerewe. Boti hizo zitakuwa ni za kisasa zenye fish finder, kwa maana kifaa maalumu kinachoelekeza wapi samaki alipo lakini pia vilevile kitakuwa nae neo la kuhifadhia samaki lisilopungua tani moja, kitakuwa na GPS na vifaa vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbili, Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa pesa takribani bilioni 20 kwa ajili ya zoezi la ufugaji wa samaki kuongeza uzalishaji wa samaki aina ya sato. Walengwa ni pamoja na vikundi vya vijana na akinamama.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana kwa kuniona. Wizara katika siku za karibuni ilitoa nafasi kwa Vikundi Mbalimbali vya Uvuvi viweze kuomba mikopo katika Wizara hiyo. Swali langu, je, ni lini fedha hizo zitatoka ili ziweze kuwanufaisha wananchi wetu wakiwemo wananchi wa Wilaya ya Kilwa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndulane, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa wanufaika wa mikopo ile ya Serikali ya Awamu ya Sita kwa Wavuvi inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan ni Wavuvi wa Kilwa, watapata boti hizo na tayari taratibu zimekwishakamilika, orodha ya wanufaika iko tayari tuta- share na Waheshimiwa Wabunge wote ili muweze kuona kile mlichokiomba ni hiki kimepatikana na kwa kusudi hilo muweze kuwafikishia walengwa wajipange ili tuweze kutekeleza kazi ya uzalishaji, ahsante sana.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwanza niipongeze Serikali kwa kutenga fedha kwa mwaka wa fedha 2018/2019 kwa ajili ya ukarabati wa majosho matano. Nilitaka kuuliza swali langu la kwanza, kama Serikali ilitenga fedha kukarabati majosho haya Matano;

Je, fedha zilizotengwa kwenda kukarabati majosho Kata ya Ngaya na Ntobo zilikwendwa wapi na kama zipo Wizarani, ni lini sasa fedha hizo zitakuja kukarabati majosho hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa tulipokea barua iliyotuonesha kwamba tutaletewa majosho Matano, na Mkeka uliotoka, kwa maana ya idadi ya majosho ya mwaka huu haijaonyesha Msalala kuwemo.

Je, ni lini sasa Wizara itatuletea majosho hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza; majosho mawili pesa zake hazifahamiki zilipo na kwa hivyo ninaomba nimueleze tu kwa mujibu wa utaratibu wa ujenzi wa majosho haya. Utaratibu wote wa manunuzi hufanywa na halmashauri ya wilaya. Baada ya kuwa wamekamilisha taratibu zote za manunuzi hutuletea Wizarani ambapo Katibu Mkuu wa Mifugo huenda kuziombea pesa zile Hazina. Ikiwa kama katika kata alizozitaja na hivyo vijiji alivyovitaja liko hilo tatizo, niko tayari mimi kumpa ushirikiano Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, kufanya uchunguzi kwa kutumia wataalam wetu ili tuweze kubaini wapi mkwamo huu ulikotokea na baadaye kuweza kuwanusuru wananchi wa pale Msalala.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni hili la kata alizozitaja ambazo zilikuwepo lakini sasa anaona katika mkeka huu wa mwaka huu hazipo. Naomba nimuhakikishie, Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan imetenga pesa za kutosha na mpaka sasa tumeshapeleka kiasi cha shilingi bilioni 5.4. Naomba nimuhakikishie tena kwa mara nyingine Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi hivi vijiji vinavyohitaji na anavyosema vilikuwepo katika mkeka nivipate tena ili tuweze kufanya ufuatiliaji wa pamoja wa kuona wapi palikosewa tuparekebishe na hatimaye wananchi wale waweze kupata ile huduma ya josho na hatimaye kuhudumia mifugo ile. Ahsante.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwenye Tarafa yangu ya Ingo yenye kata kumi na Ichuku kata tano, Inano kata tano hakuna josho hata moja katika eneo hilo. Nini mpango wa Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba Mheshimiwa Waitara aainishe mahitaji yake, ashirikiane na Mkurugenzi wake Mtendaji alete Wizarani tutamhudumia kwa jambo hili katika Bajeti ya Mwaka 2023/2024 ambayo tunaielekea sasa. Ahsante.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Wakati Mheshimiwa Naibu Waziri alipofanya ziara kule Wilayani Simanjiro aliahidi Serikali kuipatia Wilaya ya Simanjiro majosho 22 lakini mpaka sasa tumepokea majosho mawaili tu. Je, Serikali ni lini itajenga majosho katika vijiji vyote ambavyo havina kabisa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Regina, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Manyara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, maombi yalikuwa ni vijiji 22, hadi sasa wamepata majosho mawili. Mgawanyo wa majosho haya nchi nzima ni mkubwa kwa mahitaji na kwa hivyo huwa tunatenga kulingana na bajeti yetu. Haya waliyoyapata ni mwanzo na zoezi la kuendelea kupangiwa fedha linaendelea, tayari nimeshazungumza na Mheshimiwa Ole-Sendeka, alinisisitiza kuhakikisha kwamba yale yaliyosalia tuyapate. Ninataka nikuhakikishie Mheshimiwa Regina na Mheshimiwa Ole-Sendeka na Wanasimanjiro, mtapata; katika bajeti zinazoendelea kutengwa na ninyi Simanjiro mtaendelea kupata fedha hizo.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Tunaishukuru sana Serikali kwa kutenga hizi fedha milioni 400 kwa ajili ya wakulima wa mwani, lakini fedha hizi bado ni chache, hazitoshi. Wanawake wa pembezoni mwa ukanda huu wa bahari wamehamasika sana kulima mwani;

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha wanakwenda kuwaongezea fedha ili kuongeza tija katika uzalishaji wa mwani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali langu la pili, pamoja na akina mama kuhamasika kulima mwani bado kuna changamoto kubwa ya soko;

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuunganisha wakulima wa mwani pamoja na masoko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, ni kweli, na ndiyo maana katika jibu la msingi nimesema hii ni ya awamu ya kwanza; lakini awamu ya pili ambayo tayari maandalizi yake yamekwisha kukamilika ni jumla ya kiasi cha shilingi bilioni 2.5 zitaongezwa. Na kwa hili tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kwenye program hii iongezwe fedha ambayo itakawenda kuongezeka kwa vikundi kadhaa vya kina mama watakao nufaika na mkopo huu usio na riba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni changamoto ya soko. Upande wa soko unakwenda sambamba na upande wa uzalishaji. Kwa hatua tunayoiendea ya kuongeza uzalishaji imevutia wanunuzi wakubwa wengi. Hivi ninavyozungumza, ushindani juu ya ununuzi wa zao la mwani umeanza. Kampuni zimekwishafikisha bei ya mwani aina ya spinosum shilingi 900 na kwa upande wa aina ya cottonii ni shilingi 200. Kwa hiyo tunakwenda vizuri. Kwa upande wa Serikali tumejipanga kujenga maghala lakini pia vile vile kutengeneza mashine kwa ajili ya ukaushaji wa mwani, ahsante.
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana namimi kunipatia fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Tumekuwa tukishauri sana hususan sisi Wabunge ambao tunatokea mwambao wa Pwani kuhusiana na bei ndogo ya mwani.

Je, Serikali haioni haja sasa kufungamanisha mfumo huu wa ununuzi wa mwani na mfumo wa stakabadhi ghalani ili kupunguza utitiri wa wanunuzi ambao wamejipangia bei ndogo na kumuumiza mkulima wa mwani?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu la msingi nimeeleza, mkakati wetu ni pamoja na kujenga maghala. Hili la kujenga maghala ni kuelekea katika kile alichokishauri Mheshimiwa Mbunge, ya kwamba tunaweza pale mbele kwenda katika mfumo wa kuliingiza zao la mwani katika stakabadhi ghalani. Tukijenga maghala na tukaongeza uzalishaji tutafanikiwa kufika katika hatua ile aliyoishauri Mheshimiwa Juma.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Bagamoyo Kata ya Zinga, Kijiji cha Mlingotini, kuna wakulima mahiri kabisa wa mwani.

Je, ni lini Serikali itawapatia vifaa hususan boti ili waweze kufika katika maeneo ya uzalishaji kwa urahisi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Muharami Mkenge, Mbunge wa Bagamoyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tuna chama kikubwa na cha mfano cha ukulima na uchakataji wa mazao yatokanayo na mwani, kinaitwa Chama cha Ushirika cha Msichoke kilichopo Mlingotini – Bagamoyo kimeomba jumla ya fedha shilingi milioni 40. Chama hiki kitapata fedha hizi hapa karibuni kwa lengo la kununua boti itakayowawezesha kina mama wale kuingia baharini kwenda kuchukua mazao yale na vile vile kamba na taitai na zana zingine. Hongera sana Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Bagamoyo, ahsante sana.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Wizara ya Mifugo imekuwa ikitoa ahadi kwa wananchi wa Ushetu kwa ajili ya kuwajengea majosho. Hata Mheshimiwa Mpina wakati akiwa Waziri alishafika Kaya za Nyankende, Ulewe na Ubagwe akaahidi lakini utekelezaji wake mpaka sasa hivi hakuna. Nataka nipate kauli ya Serikali.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cherehani, Mbunge wa Ushetu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa Serikali imefanikiwa kupeleka jumla ya fedha shilingi milioni 540 kwa ajili ya ujenzi wa majosho katika halmashauri mbalimbali nchini, na bado kiasi cha shilingi takribani milioni 100 zipelekwe pia. Ninaamini Wilaya ya Ushetu ni miongoni mwa Wilaya ambazo ni wanufaika. Naomba mara baada ya hatua hii ya Bunge nikutane na Mheshimiwa Mbunge Cherehani aweze kunipatia orodha ya vile vijiji vyake ili niweze ku-cross check kwa ajili ya ufuatiliaji wa ujenzi wa majosho haya ya wananchi wa Ushetu.
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa mwani unatambulika duniani kwamba ni zao kubwa ambalo linawasaidia akina mama kulima lakini linaweza kutupa bidhaa kama vipodozi, vyakula na vitu vingine.

Je, Serikali haioni sasa kuanzisha kiwanda ama viwanda nchini vya kuchakata mwani ili tuweze kuzalisha bidhaa hizi ndani ya taifa letu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asya Mwadini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli mwani hutumika kwa ajili ya kutengeneza kimiminika kizito ambacho hutengenezea vipodozi, na pia vile vile hutumika kama sehemu ya kutengenezea vyakula hususan kama ice cream na vinginevyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tunao mpango wa kukutana na wazalishaji wa ndani ya nchi wanaotumia malighafi hii kwa lengo la kuwahamasisha kuingia katika utaratibu ambao utapelekea wakulima wetu waweze kuchakata na kuwauzia wao wanaotumia ndani ya nchi kama vile kampuni za utengenezaji wa vipodozi na kampuni za utengenezaji wa vyakula. Ndiyo maana katika mkakati wetu tumeweka mashine za ukaushaji na hatimaye kutengeneza mpaka katika kufikia hatua ya kuwa kimiminika kizito kitakachokwenda kutengeneza colgates na vipodozi kama vile lotions lakini vile vile kwa ajili ya kutengenezea ice creams.
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Naibu Waziri kwa kunipa majibu yake mazuri sana ambayo nimeyapokea.

Mhshimiwa Spika, Jimbo la Mtwara Mjini ndiyo Jimbo ambalo linazungukwa na bahari. Kwa namna moja au nyingine, vijana wengi wa Mtwara Mjini shughuli zao zinahusika kwenye bahari: Je, ni lini Serikali itanihakikishia kwenye vikundi zaidi ya 30 ambavyo tuliahidiwa kwamba vitapata vitendea kazi, nyavu na vitu vingine, vitasaidiwa? Nipate majibu.

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Tunazungumzia bahari kama bahari: Ni lini Serikali itatuletea meli ya uvuvi ili vijana hawa waweze kupata ajira na samaki ambao wanapotea kwa njia bahari tuweze kunufaika sasa Tanzania kama nchi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, kwanza naomba radhi kwa kutokupata majibu haya kwa ufasaha katika meza yako. Naomba nikuahidi kwamba tutafanya marekebisho ya utaratibu huu usirejee tena.

Mheshimiwa Spika, la pili, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hassan Mtenga, Mbunge wa Mtwara Mjini kwanza kwa kumpongeza kwa kazi kubwa anayoifanya hasa ile niliyotangulia kuijibu katika jibu la msingi la kuwavuta wawekezaji na kukubali kuwasaidia wana- Mtwara.

Mheshimiwa Spika, kuhusu tutawasaidiaje vijana katika vikundi hivi 30 alivyovitaja waweze kununua nyavu na injini; matarajio yetu katika bajeti inayokuja ya 2022/2023, tunao utaratibu mzuri ambao tutakaposoma bajeti yetu, nataka niwaahidi Waheshimiwa Wabunge wengi, wataona matumaini makubwa ambayo yataenda kujibu swali hili la Mheshimiwa Mtenga. Kwa hiyo, ni matarajio yetu katika mwaka ujao wa fedha, viko vikundi vya vijana vitakavyopata fursa ya kwenda kupata mikopo nafuu ambapo wataweza kununua nyavu na injini.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni juu ya ununuzi wa meli ambazo zitatoa pia ajira kwa vijana. Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ina mkakati mzuri wa kwanza kwa kujenga Bandari ya Uvuvi. Bandari ambayo itajengwa katika Mji wa Kilwa Masoko. Vilevile tunayo bajeti ya kwenda kununua meli za uvuvi zipatazo nne. Meli hizi zitakwenda kuajiri vijana wa Kitanzania wakiwemo vijana kutoka katika Jimbo la Mheshimiwa Hassan Mtenga, kwa maana ya pale Mtwara Mikindani. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa ajali nyingi za wavuvi zinazotokea baharini husababishwa na utabiri wa hali ya hewa: Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapatia taarifa za dharura wavuvi wetu kabla ya kuingia baharini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwadini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jambo hili ni jema na zuri, tumekwishalianza. Kupitia Taasisi ya yetu ya Utafiti ya TAFIRI tumetengeneza programu maalum ya kuwasaidia wavuvi, inayoweza kuwajulisha juu ya makundi ya samaki mahali yalipo. Pia programu hii itaenda mbele, itawasaidia kwenye kufafanua pia na hali ya hewa. Kwa hiyo, ni jambo ambalo tunaendelea nalo hivi sasa na tunalieneza ikiwa ni pamoja na elimu yake ili liweze kuwafaidisha wavuvi wetu.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Ni dhahiri kwamba ndani ya nchi hii nzima wameshahamasisha shule 39 tu, sasa unaweza ukajua nchi hii ina shule ngapi na sasa zimehamasisha shule 39 tu kunywa maziwa na watu waliohamasisha ni 90,000. Sasa swali langu la nyongeza ni hili.

Mheshimiwa Spika, kwakuwa Mikoa yote iliyotajwa bahati mbaya sana ni kama Mikoa mitatu, minne na Mikoa tunayo mingi tu na hasa Mkoa ninaotoka mimi Mkoa wa Geita haukutajwa.

Ni nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha maziwa mengi yanayopotea huko vijijini kwa sababu yamekosa hifadhi yanaweza kupata hifadhi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili nini mkakati wa Serikali kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya kuchakata maziwa ili tuwe na uelewa kwamba wafugaji ambao wanafuga sasa wana uwezo wa kufuga kwa tija zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bryceson Tumaini Magessa Mbunge wa Busanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mikakati yetu kama Wizara ni pamoja na kushirikiana na Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa maana ya TAMISEMI ili kuweza kutanua wigo zaidi wa kuongeza idadi ya shule. Ni kweli kwamba shule hizi tulizozisema ni chache na kwa hiyo kwa kushirikiana na wenzetu tunayo imani ya kwamba tutaongeza idadi ya shule.

Mheshimiwa Spika, namna gani ya mkakati wa kuweza kuyakusanya maziwa ya vijijini, ukitazama katika bajeti yetu ya mwaka 2021/2022 tunayoimaliza, Serikali iliondoa kodi ya vikusanyio kwa maana ya cans zile za stainless steel ambazo zilikuwa zikiuzwa takribani Shilingi 260,000, hivi sasa zinauzwa Shilingi 219,000. Hii imerahisisha kuongeza idadi ya cans za kukusanyia maziwa.

Mheshimiwa Spika, mkakati mwingine ni juu ya nini tulichonacho sasa kwa ajili ya kuongeza viwanda vidogo vya kutengeneza maziwa na kukusanyia maziwa kule vijijini. Katika mwaka huu wa fedha wa 2022/2023 katika vitu vikubwa tutakavyokwenda kuvifanya ni pamoja na kuhakikisha kwamba tunatatua zile changamoto zinazowakabili wafugaji wetu na kupelekea kushindwa kusindika maziwa yao, ikiwa ni pamoja na kuondoa tozo zile ambazo ni kikwazo.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo naomba nimuahidi Mheshimiwa Magessa yeye na Wabunge wengine wakereketwa wa viwanda vidogo wakae tayari katika kutushauri na kuweza kufikia lengo hili.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ninamshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu ya Serikali ambayo yameonesha matumaini sasa ya kuanza mchakato wa ujenzi wa Chuo cha Usafiri na Usafirishaji pale Kikwetu.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Manispaa ya Lindi tumetoa Hekari 125 bure kwa Ndugu zetu hawa wa NIT, lakini hekari 150 kwa Ndugu zetu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Kilimo pale Lindi Mjini, sasa ni miaka mitatu, ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Je, ni lini sasa Serikali itawawezesha ndugu zetu wa NIT kuwapatia fedha kwa ajili ya kuharakisha ujenzi wa chuo hiki cha Usafiri na Usafirishaji? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili tunategemea kwamba chuo cha Kilimo Kampasi ya Lindi tungependa sasa kuongeza Kitivo cha Uvuvi na masuala ya kilimo cha Mwani kutoa fursa ya ajira kwa vijana na wananchi wa maeneo hayo ya Lindi na Mtwara. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hamida Abdallah Mbunge wa Lindi Mjini. Mbunge huyu ni katika Wabunge wafuatiliaji sana wa masuala ya Wavuvi

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ni hili la lini watapewa fedha NIT. Nafikiri ni wakati mzuri ameuliza swali hili kwa sababu ni kipindi ambapo Serikali tupo katika kuwasilisha bajeti hapa Bungeni na kwa hivyo chuo cha NIT ni chuo cha Serikali na kipo katika hodhi ya Wizara zetu na hili litajibiwa wakati Wizara husika itakapokuwa ina wasilisha bajeti yake hapa.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni juu ya jambo la Kitivo ha Kilimo kuhusianisha na course za mifugo na uvuvi. Wazo na fikra aliyoitoa Mheshimiwa Hamida ni nzuri na mimi naomba niichukue kwa niaba ya Serikali ya Serikali na kwa hivyo basi tutaipeleka kwa wenzetu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kama ilivyo desturi waweze kuunganisha fani hizi nazo ziweze kutolewa pale pindi chuo kitakapokuwa tayari. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa nini Serikali inadhoofisha ustawi wa Ziwa Nyasa katika Mkoa wa Ruvuma ikiwa pamoja na kuwadhoofisha wananchi wa Mkoa wa Ruvuma hususani Wilaya ya Nyasa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Rais ametenga shilingi bilioni 20 kwa ajili ya kuendeleza Maziwa, lakini bilioni 20 hizi zote zinapelekwa katika Ziwa Victoria, je, kwa nini Serikali haiweki uwiano sahihi katika Maziwa yote haya matatu ikiwemo Ziwa Victoria, Ziwa Nyasa na Ziwa Tanganyika? (Makofi)
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa fursa hii ya kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jacqueline Msongozi.

Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu swali hili kwa ruhusa yako sekunde moja, naomba nitumie fursa hii ndani ya Bunge hili Tukufu, kumshukuru Mwenyezi Mungu na pili kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani yake kwangu na kunikabidhi kazi hii ya kuongoza Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Naomba pia niendelee pia kuomba ushirikiano kwa Waheshimiwa Wabunge wenzangu wakati wote wa kutekeleza majukumu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maswali ya Mheshimiwa Msongozi la kwanza juu ya kudhohofisha Ziwa. Nataka nimhakikishie yakwamba Serikali haina mpango wa kudhoofisha Ziwa Nyasa na katika bajeti hii ya 2022/2023 na hata katika bajeti ya 2021/2022 Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inayo mambo iliyofanya katika Ziwa Nyasa ikiwemo ujenzi wa Soko katika Jimbo la Nyasa linaloongozwa na Mheshimiwa Mbunge Engineer Stella Manyanya. Hivi sasa tupo katika hatua ya mwisho ya kukamilisha hatua za ujenzi wa soko lile ilimradi tuweze kuliruhusu liweze kutumika, lakini kama haitoshi kuhusiana na…

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, tusaidie kufupisha hayo majibu tafadhali.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jibu la pili, uwiano, katika jibu la msingi alilolitoa Mheshimiwa Naibu Waziri ambaye nampongeza kwa majibu yale mazuri, ni kwamba hatua ya mwaka huu ni hatua ya Ziwa Nyasa. Naomba Mheshimiwa Mbunge Msongozi na Wabunge wa Mkoa wa Ruvuma, lakini pia vilevile na Wabunge wa Mkoa wa Kigoma wawe na uhakika kwamba sasa zamu yao na wao inafikiwa baada ya hatua hizi za msingi kuwa zimetekelezwa ikiwa ni pamoja na Ziwa Rukwa pia vilevile litafikiwa, ahsante sana. (Makofi)
MHE. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Licha ya majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amesema kuwa wawekezaji kuingiza hizi nyavu zilizo bora wanahamasisha; je, kuna mkakati gani wa Serikali wa kuhamasisha hawa wawekezaji wanaoleta hizi nyavu badala ya kuleta wakaanzisha viwanda hapa Tanzania vya kutengeneza hizi nyavu zinazotakiwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mto Kilombero kuna wavuvi wanaovua sana sana kutoka Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi; je, kuna mpango gani wa kuhamasisha na kuwapatia nyavu bora za uvuvi? Ahsante sana.
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Morogoro kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, je tumejipangaje kwenye kuhamasisha juu ya ujenzi wa viwanda vya nyavu hapa nchini? Jambo hili tayari linafanywa na tumekwisha kuanza kupata viwanda ambavyo vinatengeneza nyavu. Pale Mwanza tunacho kiwanda kipya kinaitwa Ziwa Net ambacho kinatengeneza nyavu na kuwauzia wavuvi na tunayo maombi pia vilevile ambayo tunashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa ajili ya uwekezaji kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ni suala la zana kwa ajili ya wavuvi kwenye mto Kilombero. Jambo hili nimelichukua kama ombi la Mheshimiwa Mbunge, Dkt. Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum na nitakwenda kuzungumza naye ili kuweza kuandaa wavuvi wa Mto Kilombero katika vikundi na baadae na wao ikiwezekana waweze kupata hizi zana kama ambavyo wanapata wavuvi wengine nchini.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza.

Wananchi wa Mtaa wa Bangulo kwenye Kata ya Pugu Station walikuwa na mgogoro na shamba la Kabimita ambao Serikali iliumaliza kupitia Mawaziri wa Ardhi na Mifugo mwaka 2018 lakini mpaka leo wananchi wamefanya urasimishaji na Kabimita kupitia Wizara ya Mifugo haijakabidhi hati ya eneo hilo.

Je, ni lini sasa Serikali itaenda kukabidhi hati hiyo kwa Kamishina wa Ardhi ili wananchi wa Mtaa wa Bungulo Kata ya Pugu Station waweze kukabidhiwa hati yao na kuishi kwa amani?
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Ukonga ka,a ifuatavyo:-

Ni kweli kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan juu ya kutatua migogoro tayari jambo hili tulikwishafika mwisho na Mheshimiwa Jerry kama ambavyo nimemjibu Mheshimiwa Massare katika swali la awali ni kwamba utaratibu wote ulikwisha kufanyika, wananchi wote ambao wanapaswa kupewa haki wanafahamika nani hatua tu za Kiserikali.

Sasa nitamwelekeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Kamishina wa Ardhi, jambo hili lifike mwisho na hatimaye hati iweze kuwa surrendered na wale ambao wanapaswa kunufaika, wanufaike na kama kuna malipo ya premiums ambazo wanatakiwa kufanya, wanatakiwa wafanye sawa na Sheria za Ardhi zinavyoelekeza, ahsante sana.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Waziri mwaka 2016 Serikali iliwekeza fedha kwenye mwalo wa Kirando wenye thamani ya shilingi bilioni 1.1. Lakini mwaka 2019 mwalo huo ulizama ikiwepo Kasanga pamoja na maeneo mengine yote ya Ziwa Tanganyika. Nataka kujua Serikali ina mkakati gani wa ziada wa kujengwa mwalo mwingine na kuupandisha hadhi kama ulivyosema kwenye Kata ya Kirando?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ili kunufaika na mazao yatokanayo na uvuvi kwenye ushindani wa soko ni lazima Serikali iwekeze kwenye kulinda mazalia ya samaki. Napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa ziada wa kulinda mazalia ya samaki bila kuathiri wavuvi wetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza Serikali imeshatoa maelekezo kwa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kupendekeza maeneo wanayodhani kuwa yanaweza kufaa sasa mara baada ya maji kuingia katika mwalo ule wa mwanzo, na mara baada ya kupendekeza tutakuja kufanya tathmini ili tujiridhishe na mchakato sasa wa ujenzi uweze kuanza.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili juu ya mazalia; mazalia ya samaki nini mkakati wetu ni kwamba Serikali la kwanza kwa kushirikiana na jamii tuko tayari na tunajipanga katika kuyatambua, kuyaainisha na kuyatangaza kwa mujibu wa sheria ili baadae tuweze kuyalinda na naomba niihase jamii ya wavuvi maeneo yote nchini ya kwamba kazi ya kulinda rasilimali hizi hususan maeneo ya mazalia ni kazi ya jamii nzima, Serikali za Vijiji, Serikali za Kata, Serikali mpaka Wilaya na Mikoa ni kazi yetu sote Watanzania.

Mheshimiwa Spika, bila ya kulinda mazalia samaki wetu watakwisha na hatua kali tutaichukua kwa yeyote anayefanya maingilio ya kwenda katika kufanya kazi ya uvuvi kwenye eneo la mazalia. Huo ni uhalifu na hatutamvumilia yeyote ambaye atakwenda kuharibu rasilimali hii ya Watanzania.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nashukuru kwa majibu haya mazuri; lakini kwa kuwa Serikali imeelemewa sana na jambo hili, ina mpango gani sasa au ina vivutio gani kwa sekta binafsi kuzalisha mbegu hizo za malisho pamoja na kuzalisha madume bora ya mbegu? (Makofi)

Swali la pili kwa kuwa kuna uhitaji mkubwa sana wa mitamba bora, mbuzi mapacha, pamoja na vifaranga vya kuku vilivyoboreshwa kwa wanawake wa Mkoa wa Kilimanjaro ambao wanasubiri kwa muda mrefu hata wakati wa kampeni walimuomba Waziri Mkuu alipokuja kufungua kampeni ya Mkoa wa Kilimanjaro. Serikali iko tayari sasa kutoa vitu hivyo kwa ruzuku kwa wanawake hao?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shally Josepha Raymond, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza ni juu ya vivutio tulivyoviweka; Serikali imejipanga mara baada ya kupokea maoni ya wadau juu ya kuweza kuweka vivutio kwenye upande wa uzalishaji wa mbegu za malisho, lakini na upande wa uzalishaji wa ng’ombe bora kwa maana ya madume ya mbegu kwa kuondoa baadhi ya tozo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa ng’ombe bora Serikali imeondoa tozo ya import ya ng’ombe wanaotoka nje ya nchi tulikuwa tukilipisha shilingi 10,000 kwa ajili ya ng’ombe kumkagua na sasa Wizara imependekeza kuondolewa kwa tozo hii na bado tupo katika mazungumzo ndani ya Serikali ya tozo kwa upande wa mbegu za kutoka nje za malisho ili kusudi na zenyewe ikiwezekana ziweze kuondolewa ile tozo na wawekezaji waweze kuweza kufanya kazi hii kwa ufasaha.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni juu ya jambo linalohusu Mkoa wa Kilimanjaro na akinamama kupata ng’ombe wa ruzuku. Katika mwaka huu wa fedha 2022/2023 Serikali imejipanga kuyaimarisha mashamba ya uzalishaji wa ng’ombe bora na ili tuweze kuwasambaza kwa wafugaji kote nchini. Nina imani kuwa akinamama wa Mkoa wa Kilimanjaro watakuwa ni miongoni mwa wanufaika, ahsante sana.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi; Serikali ina mpango gani wa kuimarisha Shamba la Mifugo la Kitulo wilaya ya Makete na shamba la mifugo la Sao Hill Iringa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Njombe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 tumedhamiria kuhakikisha kwamba tunaimarisha mashamba yetu matano likiwemo hili la Kitulo na lile la Mabuki na Sao Hill ambayo tutayaongezea zana za kazi kama vile matrekta na zana zile za kuweza kuvunia majani kwa maana ya malisho, lakini pia vilevile kwa kuyaongezea ng’ombe wazazi bora ili tuweze kuzalisha zaidi ya ng’ombe 3,500 na kuwasambaza nchini kote, kwa hivyo, mpango huu tunao na tunaelekea katika kuutekeleza, ahsante sana. (Makofi)
MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Swali langu la nyongeza ni kwamba nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Je, Pamoja na juhudi nzuri walizofanya kuhakikisha zao la mwani linakuzwa.

Je, Serikali imefanya juhudi gani kuhakikisha wakulima hawa wanapata soko ambalo litakidhi haja ya kilimo chao?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Said Issa Mbunge wa Konde kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya jitihada ya kutafuta masoko na kwa sasa tuna masoko katika nchi za Marekani, Ufaransa na Spain. Kwa umuhimu zaidi tumeanza mazungumzo na Shirika la Usafirishaji, Tumeanza mazungumzo na shirika la usafirishaji la DHL ili kuweza kuhakikisha kwamba wazalishaji kwa maana ya wakulima wanapata masoko Kimataifa moja kwa moja kwa kuwa tumeshapata kujua juu ya nini soko linahitaji, mawasiliano ya moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, hatua ya pili tunashukuru katika bajeti ya mwaka huu tunaouendea 2022/2023 Serikali imetenga fedha za kutosha za kuhakikisha wakulima wanaongeza thamani ya zao hili. Kwa hivyo, tutakuwa na mashine za ukaushaji wa Mwani katika mwambao wote wa Pwani, kuanzia Tanga, Pwani mpaka Lindi na Mtwara kwa lengo la kuhakikisha tunaongeza thamani ya zao letu la Mwani ili tuweze kulingana na mahitaji ya soko. Ahsante sana.
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na mimi kunipatia fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Kwa vile zao hili la Mwani zaidi ya asilimia 80 ndiyo tunategemea mauzo ya nje, lakini zaidi ya asilimia 20 ndiyo inabakia kwa ajili ya kulichakata na kutengeneza bidhaa mbalimbali ambazo zinabaki ndani ya nchi. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutoa elimu hasa kwa wale wakulima wetu ndani ya nchi kuweze kutengeneza bidhaa ambazo zitakuwa na soko pia zitakuwa na quality pia zitakuwa zinauzika ndani ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamad kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, juu ya mpango wa Serikali wa kuhakikisha kwamba tunaongeza thamani kama nilivyokwisha kueleza kwenye jibu la msingi. Kwanza Mwani wetu mwingi unakaushwa katika michanga, Mheshimiwa Hamad na Wabunge wa kutoka katika Mikoa hii ya huku Pwani inayolima Mwani wanaweza kuwa ni mashahidi wangu. Ndiyo maana tumejielekeza katika kuhakikisha kwamba tunapata kitu kilicho na ubora kwa kwenda kupeleka mashine za kukausha huu Mwani ili kusudi twende katika hatua inayofuata sasa ya kuongeza thamani kutengeneza sabuni, shampoos, bidhaa za chakula kwa ajili ya kuongeza hii thamani. Kama haitoshi, mbele zaidi tunataka tuanze kufanya extraction.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri ngoja ngoja kwa sababu muda wa kujibu swali ni mfupi, anataka kujua mpango wa elimu kwa hao wakulima wa Mwani.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, shukrani sana. Kama nilivyoeleza katika jibu la msingi elimu tayari ilishatolewa na tunaendelea kutoa. Kwa hivyo, tutaendelea na mpango wa utoaji wa elimu katika vikundi vyote tunawaunganisha wakulima wa Mwani ili kuweza kuwa rahisi kwa kazi yetu ya utoaji wa elimu katika Mwambao mzima wa Ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi. Ahsante.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa vile wanaojishughulisha sana na zao la Mwani ni wanawake. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapa wanawake hao nyenzo za kisasa kwa ajili ya kilimo hicho?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tulishakwisha kuanza kutoa zana kama vile Kamba na ipo zana inaitwa taitai na hilo zoezi tutaendelea nalo ikiwa ni pamoja na matarajio yetu ya kununua boti ambazo zitakwenda kwa ajili ya wavuvi lakini na vikundi vya akina mama kwa ajili ya wakulima wa Mwani kuweza kuyafikia maeneo yale pale maji yanapokuwa mengi na uvunaji wa ule Mwani. Ahsante sana.