Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hamoud Abuu Jumaa (28 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nichuke fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha kusimama kwenye Bunge lako Tukufu kwa mara nyingine, lakini pia niwashukuru wananchi wangu kwa sababu ndio ninasimama kwa mara ya kwanza, kwa kunirejesha tena bungeni kwa kipindi cha pili.
Vilevile nichukue fursa hii kukupongeza wewe kwa kazi kubwa ambayo unayoifanya hapa bungeni, waswahili wanasema; kuvuja kwa pakacha nafuu ya mchukuzi; lakini wanasema raha tele, taabu ya nini? Lakini pia wanasema kwa nini uminyane na ukuta wakati malango upo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza nichukue fursa hii na mimi niipongeze Serikali kwa maana ya Waziri, Naibu Waziri na wataalam wake wote kwa kuandaa bajeti nzuri yenye lengo kubwa la kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2016 na hii imeonesha ushahidi hata katika kutenga bajeti ya maendeleo kwa mara ya kwanza tumetenga bajeti takribani asilimia 40. Hii yote inaonesha dalili njema ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM. Naamini fedha hizi zikienda vizuri na tukisimamia vizuri sisi Wabunge tunaweza tukafanya mambo makubwa zaidi, na hatimaye tukaleta maendeleo makubwa; na baadaye katika uchaguzi wa mwaka 2020/2025 tukapata kura nyingi na Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi upo uwezekano mkubwa wa kuendelea kushika dola. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, ningependa kuchangia katika suala zima la mabasi ya mwendokasi, lakini vile vile niipongeze Serikali kwa kuanzisha mpango huu wa mabasi ya mwendokasi japo kuwa ziko changamoto mbalimbali ambazo zinajitokeza na sisi wote mashahidi, lakini niseme tu jambo hili zuri na nichukue fursa hii kumpongeza Waziri Mkuu na wote mashahidi tumeona amekwenda kupanda basi lile, Makamu wa Rais, Rais Mstaafu, ni jambo jema na ndio maana wanatamani na watu wengine waweze kwenda kupanda mabasi. Ziko changamoto mbalimbali, sisi wote mashahidi tunaona, kuna watu mbalimbali ambao wanavunja sheria, magari yanaigia katika njia ile ambayo hayaruhusiwi. Sasa ushauri wangu tuangalie Serikali ni jinsi gani ya kutunga sheria nyingine kali zaidi ili kusiingie tena na uharibu ambao mradi huu umeingia gharama kubwa na tumetumia pesa nyingi sana katika kuutekeleza mradi huu.
Lipo jambo lingine ninaloshauri, maana ya mabasi ya kwenda kasi, tungetafuta utaratibu, kwa mfano tungeanzisha basi lingine au mawili, matatu basi moja linatoka Kimara, linakwenda mpaka Posta, na lingine linatoka Posta mpaka Kimara. Pale Italy ipo moja treni inaitwa rapido ni treni ambayo inakwenda kwa spidi, sasa tukianzisha mabasi haya ya kwenda kasi mawili ili watu waweze kwenda kwa haraka zaidi, hata tukiongeza gharama kidogo itasaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tusiishie hapo, mabasi yale sasa hivi yamesaidi kwa kiasi kikubwa kupunguza foleni Dar es Salaam na sisi wote mashahidi. Tungeanzisha kujenga hata yard pale moja ya kuegesha magari, kuna watu wanatoka maeneo mbalimbali, inawezekana wakaja pale wakaegesha magari yao, na baadaye wakapanda mabasi wakaenda Posta, mjini wakafanya shghuli zao na baadae wakarudi katika shughuli hizi za kawaida. Ili twende vizuri zaidi, Serikali ilikuwa na mpango wa kujenga barabara ya njia sita kutoka Dar es Salaam kwenda mpaka Chalinze na baadaye kuelekea Morogoro. Naishauri mpango huu ufanywe haraka ziaidi tukijenga barabara ya njia sita itatusaidia sana kupunguza foleni. Kwa sababu leo ukitokea Dodoma, Morogoro na kuelekea Dar es Salaam ukifika Kibaha hapo katikati kuna kuwa na foleni kubwa. Kwa hiyo, tukijenga barabara ya njia sita itapunguza kwa kiasi kikubwa foleni za magari ili tuende vizuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, liko suala limezungumziwa sana na wenzangu suala la zima la CAG. CAG ameomba karibuni takribani shilingi bilioni 88 lakini pesa aliyopewa takribani shilingi bilioni 44; pesa hizi ndogo sana, nashauri na wenzangu wengi wamelizungumzia kwa kasi kubwa, naomba tu Serikali iangalie ni jinsi gani ya kuongeza fedha hizi kwa CAG ili tuweze kufanya kazi vizuri. Kwa sababu huyu ndio mwangalizi wetu akipata fedha ndogo hizi atashindwa kufanyakazi yake vizuri, kwa hiyo, naomba aweze kupata pesa hizo ziweze kwenda vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namba tu ni-declare interest mimi na Mheshimiwa Zungu wavaaji wazuri sana wa mitumba, sasa katika eneo hili naona mmeongeza kodi kubwa ya mitumba…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuweza kunifikisha mahali hapa na mimi leo hii niweze kuchangia hoja hii muhimu iliyopo mbele yetu. Napenda vilevile kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuandaa hotuba nzuri ya bajeti yenye mlengo chanya kwa mafanikio, maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii inatupa mwelekeo wa kazi za Serikali na makadirio ya fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge, hakika ni mwelekeo mzuri na wa kupongezwa sana, kwani imezingatia Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015. Nichukue
nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kufanya ziara maeneo mbalimbali na nimshukuru pia kwa kufanya ziara jimboni kwangu Kibaha Vijijini, ziara zake zimekuwa na tija kubwa sana kwa maendelo ya wananchi, na kufungua fursa mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia fursa hii kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali ilizochukua kwa maendeleo ya Taifa letu, hatua ya kuhamia Dodoma na kuwa Mji Mkuu wa nchi yetu ni hatua nzuri na ya kuthubutu, kwani maamuzi yalishafanywa hapo awali na ilikuwa bado
utekelzaji tu. Yatupasa kuunga mkono jitihada hizi na kuishauri Serikali kwa namna yoyote katika uboreshaji wa mkakati huu ambao tayari umeshaanza kwa Wizara mbalimbali kuhamia Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kila mpango huja na changamoto zake, vivyo hivyo katika mpango huu wa kuhamisha Makao Makuu ya nchi yetu kuja Dodoma unachangamoto mbalimbali, changamoto hizi ni pamoja na mipango miji, barabara na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Dar es Salaam na miji mingine leo hii tunaona kwa namna gani tulichelewa katika kupanga miji yetu na leo hii miji haijapangika, tumekuwa na changamoto mbalimbali ambazo ni wajibu wetu kuzichukua kama fursa na kuja nazo Dodoma na kuziboresha hivyo kuepuka makosa yaliyofanyika katika miji mingine hususan mji wetu wa Dar es Salaam hayana budi kutokutokea katika Mji wetu wa Dodoma. Mipango Miji ipangwe vizuri, kutengwe maeneo ya viwanda, makazi ya watu, ibada, vituo vya mafuta, shule, hospitali, viwanja vya michezo na kadhalika, pia barabara zitengwe maeneo makubwa na ya kutosha ili kuepuka bomoa bomoa za kila mara ambazo tumekuwa
tukizishuhudia katika miji mbalimbali, mji wa Dodoma uwe ni mji wa mfano na wa kihistoria, mitaro ya kupitisha maji (drainage system) iboreshwe kikamilifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwa kufanikiwa kwa kiasi kikubwa mpango wa kutoa elimu bure wenye tija kubwa kwa wananchi wetu ili kila mtoto wa Kitanzania aweze kupata elimu. Uwajibikaji na nidhamu katika utumishi wa umma
umekua kwa kiasi kikubwa ikilinganishwa na hapo awali ingawa bado zinahitajika juhudi zaidi kufanywa na Serikali ili hii dhana ya uwajibikaji iwe endelevu na yenye tija zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, bado tuna changamoto ya upatikanaji wa huduma mbalimbali kwa wananchi. Napenda kuishauri Serikali yangu sikivu kuzichukua changamoto hizi kama fursa kwa kuboresha maeneo hayo kwa maendeleo ya wananchi wetu na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kugusia suala zima la ukuaji wa uchumi nchini. Serikali imeainisha ukuaji wa uchumi kwa mwaka 2016/2017 unaonesha uchumi wetu unazidi kuimarika. Kwa takwimu za Ofisi ya Taifa ya Takwimu, ukuaji halisi wa Pato la Taifa ulifika 7.0% mwaka 2016, pongezi kwa Serikali ila kuna changamoto nyingi sana katika ukuaji wa uchumi kwa ujumla na ukilinganisha na uchumi wa mtu mmoja mmoja, wananchi wengi ambao vipato vyao ni vidogo na maskini wamekuwa wakiendelea kulalamika hali ngumu ya maisha, mifumuko ya bei za bidhaa muhimu kama chakula na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ikiwaumiza sana wananchi na hivyo kutokuona umuhimu wa hizi takwimu za ukuaji ama nafuu ya maisha. Naomba kuishauri Serikali kuwajengea uwezo wananchi ili waweze kukabiliana na changamoto hizi wanazokumbana nazo, Serikali iweze kusimamia vyema mifumuko ya bei isiyokuwa na tija na yenye kumuumiza mwananchi wa kawaida. Serikali isimamie kikamilifu bei za mazao ya wakulima ambao ndio nguvu kazi kubwa hapa nchini, wauze mazao yao kwa faida ya bila vipingamizi vyovyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mdogo ni Serikali ilipoamua kusimamia bei la zao la korosho na kufanikiwa kwa kiasi kikubwa kwa wakulima kuuza mazao yao kwa faida nzuri. Hivyo naiomba Serikali ifanye pia katika mazao mengine nchi nzima ili wakulima wetu ambao kitakwimu
ndio wengi waweze kufaidika na kilimo, waondokane na umaskini na kuona faida hizi za ukuaji wa uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishazungumza sana na kuchangia humu Bungeni kwa umakini mkubwa na kuishauri Serikali kuwa viwanda ndio msingi mkubwa wa ukuaji wa uchumi na kumaliza kama si kupunguza tatizo la ajira. Naishukuru Serikali ya Awamu ya Tano ikiongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli kuja na kipaumbele hiki cha Tanzania ya viwanda. Na mimi nasema Tanzania ya viwanda inawezekana kwa kuungana sote na kuunga mkono jitihada hizi kwa manufaa ya nchi yetu ili tuondokane na changamoto nyingi tunazokabiliana nazo za ajira kwa vijana wetu ni lazima tuwekeze katika viwanda kwani malighafi mbalimbali tunazo hapa hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi nyingi tajiri kiuchumi duniani ni maamuzi ya uwekezaji wao katika viwanda kwa muda mrefu. Mkoa wetu wa Pwani una viwanda takriban 89, viwanda hivyo viko katika maeneo mbalimbali ya mkoa lakini mpango kazi wetu ni kuzidi kutafuta wawekezaji ili waje kuwekeza katika mkoa wetu hususan Kibaha vijijini kwani tuna maeneo makubwa yametengwa kwa ajili ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto mbalimbali katika sekta ya viwanda hususan katika utoaji wa vibali vya mazingira. Nashauri vibali hivyo vya mazingira viwe vinatolewa kwa eneo zima ili kuepuka usumbufu wa mtu mmoja mmoja kufanya maombi ya vibali hivyo. Kibaha
Vijijini kama nilivyosema hapo awali tuna maeneo ya kutosha ambayo tayari yameshatengwa kwa shughuli husika. Niliishauri Serikali humu humu Bungeni kuhusu suala la bandari kavu iliyopo Kwala, bandari hii iwe maalum kuegesha magari yote (used), kwa maana kuziondoa yard za kuuzia magari (used) ambazo zimezagaa kila kona ya Jijini Dar es Salaam na hivyo kuwepo sehemu maalum ya mtu akitaka magari (used) anajua wapi pa kwenda hili limefanyika katika nchi nyingi sana zilizoendelea kama Dubai na kadhalika, huwezi kukuta kila kona ya mji kuna yard ya kuuzia magari. Hizi yard zimekuwa zikiharibu mandhari ya miji yetu na uchafuzi wa mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hilo pia la bandari kavu kuwepo na upatikanaji wa spare tofauti tofauti za magari pamoja na mashine mbalimbali. Hiyo itapelekea kuondokana na maeneo ya mijini kutapakaa maduka ya spare hovyo kama ilivyo hivi sasa mtaa wa Shaurimoyo.
Hatua hii ikikamilika watu watajua wakitaka magari yaliyotumika yote ama spare zote basi wanakwenda Kwala Kibaha Vijijini na kufanya manunuzi. Itasaidia kuwa na sehemu moja tu ambayo utapata hitaji lako ama gari au spare.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili, Serikali tayari imeshaonyesha nia kwa kutenga maeneo kama ilivyo jimboni kwangu. Kilichobaki ni utolewaji wa elimu na uhamasishaji kwa sekta binafsi kuziona fursa hizi na kuzifanyia kazi. Hatua hii ikishakamilika Serikali itapata fursa ya kuanzisha njia ya treni kutoka Dar es Salaam mpaka Kibaha kuwarahisishia wananchi watakaokuwa wakienda bandari kavu hiyo. Serikali kupata fedha za uendeshaji, vilevile Mkoa wa Pwani hivi sasa umekuwa na watu wengi sana. Kupatikana kwa usafiri wa treni hiyo kutawasaidia watu wengi sana kutatua changamoto ya usafiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilio changu cha muda mrefu ni miundombinu ya barabara na mambo mengine mengi, ila kuna hii barabara ya Makofia, Mlandizi na Mzenga ina miaka sita sasa tunazungumzia ujenzi wa barabara hii. Wananchi wamekuwa wakipata shida sana katika shughuli zao za kila siku kutokana na hii barabara, shughuli zao za kiuchumi zimekuwa zikizorota. Naiomba Serikali hii sikivu sasa katika bajeti hii wakamilishe ujenzi wa barabara hii. Wananchi wale na wao waone faraja na kuanza kutumia barabara nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti hii tunaomba fedha zitengwe na barabara hiyo iweze kukamilika. Hata hivyo, niipongeze Serikali kwa jitihada kubwa zinazoendelea kuzifanya kwa kuleta miradi mikubwa ya barabara za juu makutano ya TAZARA, daraja jipya la Salender, ujenzi wa barabara Dar es Salaam – Chalinze kiwango cha express way bila kusahau ujenzi wa barabara za juu (interchange) kwenye makutano ya barabara ya Ubungo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni hatua muhimu za kimaendeleo katika kukabiliana na changamoto ya msongamano wa magari. Vilevile Mji wa Mlandizi kutokana na kukua kwa kasi, kuna uhitaji wa makutano ya barabara ili kurahisisha watumiaji na kuufanya uwe wa kisasa zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa jitihada kubwa inazochukua katika kulinda na kufuatilia sekta nzima ya madini. Hatujachelewa bado na jitihada zilizoanzishwa na Mheshimiwa Rais ni mwanga tosha kwa sasa. Kazi imeanza na kama kulikuwa na upotevu wowote wa madini yetu au ukwepaji wa kodi sasa kila kitu kitakuwa wazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuunda Tume Maalum ya kufuatilia suala zima katika sekta ya madini. Kama tutaitumia vizuri, basi Taifa litanufaika sana na kupata maendeleo katika nyanja mbalimbali hapa nchini. Madini ni kitu ambacho hakipatikani kila sehemu au nchi madini ni bidhaa adimu sana, hivyo tukifanya maamuzi katika utulivu wenye tija basi hatua stahiki zichujuliwe na hizo
changamoto tuzichukue kama fursa na kusonga mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusimamie madini yetu yote kwa uadilifu mkubwa, zaidi madini ambayo hayapatikani sehemu yoyote duniani zaidi ya hapa kwetu tuyape thamani na kuyasimamia kwa faida ya Taifa letu ili pato la kodi liweze kuongezeka na kuleta maendeleo kwa wananchi. Vivyo hivyo, tuwawezeshe wachimbaji wadogo wadogo kwa kuwatolea kodi kwa vifaa watavyoagiza ili kuwapa motisha katika kazi zao za uchimbaji. Tuwathamini wazawa ambao ni wachimbaji wadogo kwani wametengeneza ajira hivyo kutokuwapa kipaumbele wao na kuwapa wageni tunawakatisha tamaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya wafugaji na wakulima imeendelea kuibuka maeneo mbalimbali nchini na chanzo cha migogoro hiyo ni ardhi ambayo imekuwa ikigombaniwa. Naipongeza Serikali kwa jitihada zake katika kutatua na kupambana na migogoro hiyo, ila naishauri
Serikali kupitia watumishi wake, maafisa mifugo kuanza kutoa elimu kwa wafugaji kufanya ufugaji wa kisasa ambao hauhitaji kuwa na kundi kubwa la ng’ombe ambao baadaye madhara yake mfugaji anashindwa kuwa na chakula cha kujitosheleza na hivyo kupelekea migogoro kuibuka, kutoa elimu kwa wafugaji kulima nyasi zao wenyewe na kuzihifadhi vizuri ili kipindi cha kiangazi waweze kuzitumia nyasi hizo. Kufanya hivyo kutapunguza sana hii migogoro na kurudisha hali ya kuaminiana na kupendana baina ya wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu sasa umepita tangu kuomba kuwekewa kivuko cha kuvukia watu na usafiri, Ruvu Station, Soga, Mpiji, Kwala, Magindu, kukosekana kwa vivuko hivyo kunapeleka wananchi kuwa katika hali ya hatari sana kwani maeneo hayo hayana alama
yoyote. Kwa kuwa kikwazo kwa wananchi kufanya shughuli zao za kila siku pindi wanapotaka kuvuka ama kuvusha vitu mbalimbali. Naomba katika bajeti hii sasa tupewe kipaumbele kwa maeneo hayo kuwekewa vivuko, vilevile kuna uhitaji mkubwa sana kwa maeneo tajwa hapo kuwa na vituo vya treni ili kuwarahisishia wananchi hawa pindi kukiwa na vituo kutakuwepo na fursa mbalimbali maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya mawasiliano bado imekuwa kubwa hapa nchini kwetu. Jimboni kwangu Kibaha Vijijini ni wahanga wa changamoto hii kwani kuna maeneo mengi hakuna kabisa mawasiliano ya simu kwa kuwa hakuna hata kampuni moja ya simu inayopatikana maeneo hayo. Dutumi, Mpelamumbi, Miyombo, Gwata, Msua hakuna mawasiliano kabisa. Tunaomba minara ya Tigo, Vodacom na Airtel, hakika kwa wananchi wangu hii imekuwa ni kero ya muda mrefu sana. Hata hivyo, naipongeza Serikali kwa hatua yake nzuri ya
kukamilisha kituo kimoja cha kuhifadhia taarifa na mifumo ya Serikali (Government Data Centre) na Serikali haina budi kuzihamasisha Ofisi za Serikali kutumia mfumo huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Awamu zote nilizokuwepo humu Bungeni, nimekuwa nikilisema hili la Kituo cha Afya Mlandizi kupandishwa hadhi. Sifa na vigezo tunavyo. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne na Awamu ya Tano walitoa ahadi ya kukipandisha hadhi kituo hiki na kuwa
hospitali. Lakini Awamu ya Nne imepita bila kituo hiki kupandishwa hadhi. Sasa tuko Awamu ya Tano, naomba ahadi hii sasa itekelezwe kwani Mheshimiwa Rais akitoa ahadi, kinachofuata ni utekelezaji kwa mamlaka husika. Hivyo, mimi na wananchi wangu tungeshukuru sana katika
bajeti hii maombi yetu ya muda mrefu na ahadi za Marais wawili zilitekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nimeona bajeti ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mwaka 2015/2016 hadi shilingi bilioni 251 mwaka 2016/2017. Ni jambo jema na la kupongezwa ila rai yangu kwa Serikali na mamlaka husika kumekuwa na changamoto za upungufu wa dawa katika vituo vyetu vya afya, zaidi dawa kuchelewa kufika kwa wakati. Naamini kwa ongezeko la bajeti basi changamoto hizi hazitakuwepo tena na kuleta nafuu kwa wananchi kupata dawa kwa wakati na kuwaondolea usumbufu wa kukosa dawa pindi wanapoandikiwa dawa hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama yetu ya Kibaha Vijijini ina changamoto mbalimbali ila kubwa zaidi ni jengo. Jengo lake haliko katika hali nzuri. Katika michango yangu kila mwaka humu Bungeni, mbali na jitihada zangu binafsi za kuonana na Waziri mhusika nimekuwa nikilizungumzia takriban miaka sita bila matumaini yoyote. Naomba Serikali katika bajeti hii basi ituangalie kwa jicho la huruma na sisi tupate jengo la Mahakama. Napenda pia kuikumbusha Serikali kufikisha fedha za bajeti kwa wakati katika Halmashauri zetu kwani bajeti inapita lakini fedha zinachelewa na kuzorotesha shughuli za kimaendeleo. Fedha zikifika kwa wakati na miradi ya kimaendeleo itawafikia wananchi kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, napenda kugusia kidogo suala zima la vita dhidi ya dawa za kulevya. Hili ni janga kubwa kitaifa na duniani kote. Dawa za kulevya zimekuwa zikiwaathiri hasa vijana wetu, nguvu kazi ya Taifa. Ndoto za vijana hawa zimekuwa zikisitishwa na kujiingiza katika kutumia dawa hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, napenda kuchukua fursa hii kuipongeza na kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuonyesha dhamira ya dhati kabisa ya kupambana na vita hii. Kwanza kwa kuteua watendaji wakuu watakaosimamia Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya. Mamlaka hii ina nguvu ya kukamata, kupeleleza na kushtaki watuhumiwa wanaohusika na biashara ya dawa za kulevya. Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa uwezo wake mkubwa na upendo alionao juu yetu sisi sote kwa kutuwezesha kuwa mahali hapa katika kutimiza majukumu yetu ya kila siku, pia kuniwezesha nami kuchangia hotuba hii ya bajeti iliyo mbele yetu ya mwaka wa fedha 2017/2018. Vilevile nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara kwa ujumla wake kwa kuandaa bajeti nzuri yenye mlengo chanya, bajeti hii inaenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, mahsusi kuleta maendeleo kwa wananchi wake na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilio changu cha muda mrefu ni miundombinu ya barabara na mambo mengine mengi, ila kuna hii barabara ya Makofia - Mlandizi - Mzenga, ni miaka sita (6) sasa tunazungumzia ujenzi wa barabara hii, wananchi wamekuwa wakipata shida sana katika shughuli zao za kila siku. Kutokana na hii barabara kuwa mbovu shughuli zao za kiuchumi zimekuwa zikizorota. Naiomba Serikali hii sikivu katika bajeti hii wakamilishe ujenzi wa barabara hii ili wananchi wale na wao waone faraja na kuanza kutumia barabara nzuri. Katika bajeti hii tunaomba fedha zitengwe na barabara hiyo iweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, niipongeze Serikali kwa jitihada kubwa inazoendelea kuzifanya kwa kuleta miradi mikubwa ya barabara za juu makutano ya TAZARA, daraja jipya la Selander, ujenzi wa barabara ya Dar es Salaam - Chalinze kwa kiwango cha expressway na bila kusahau ujenzi wa barabara za juu (interchange) kwenye makutano ya barabara ya Ubungo. Hizi ni hatua muhimu za kimaendeleo katika kukabiliana na changamoto ya msongamano wa magari. Vilevile Mji wa Mlandizi kutokana na kukua kwa kasi, kuna uhitaji wa makutano ya barabara ili kurahisisha watumiaji na kuufanya uwe wa kisasa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda mrefu sasa umepita tangu kuomba kuwekewa kivuko cha kuvukia watu pamoja na vyombo vya moto, Ruvu Station, Soga, Mpiji, Kwala na Magindu. Kukosekana kwa vivuko hivyo kunapelekea wananchi kuwa katika hali ya hatari sana kwani maeneo hayo hayana alama yoyote na kuwa kikwazo kwa wananchi kufanya shughuli zao za kila siku pindi wanapotaka kuvuka ama kuvusha vitu mbalimbali. Naomba katika bajeti hii sasa tupewe kipaumbele kwa maeneo hayo kuwekewa vivuko. Vilevile kuna uhitaji mkubwa sana kwa maeneo tajwa hapo juu kuwa na vituo vya treni ili kuwarahisishia wananchi hawa, pindi kukiwa na vituo kutakuwepo na fursa mbalimbali katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya mawasiliano bado imekuwa kubwa hapa nchini kwetu. Jimboni kwangu Kibaha Vijijini ni wahanga wa changamoto hii kwani kuna maeneo mengi hakuna kabisa mawasiliano ya simu. Kwa kuwa hakuna hata kampuni moja ya simu inayopatikana maeneo hayo ya Dutumi, Mpelamumbi, Miyombo, Gwata na Msua. Tunaomba minara ya Tigo, Vodacom na Airtel maana hakuna mawasiliano kabisa. Hakika kwa wananchi wangu hii imekuwa ni kero ya muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, naipongeza Serikali kwa hatua yake nzuri ya kukamilisha Kituo Kimoja cha Kuhifadhia Taarifa na Mifumo ya Serikali (Government Data Centre) na Serikali haina budi kuzihamasisha Ofisi zote za Serikali kutumia mfumo huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa sijatenda haki kama nisipoipongeza Serikali kwa hatua yake iliyoichukua siku si nyingi ya kuanza mradi mkubwa kabisa wa treni ya umeme ama treni iendayo kasi kama wengi walivyozoea. Huu ni mradi mkubwa na wa kihistoria katika nchi yetu. Mradi huu utarahisisha sana usafirishaji kwenye sekta ya reli, utapunguza muda wa kusafirisha mizigo na abiria kwani treni hii itakuwa inatumia muda mfupi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu na maombi kwa Wizara, naomba mradi huu usiache kuwajali vijana wetu katika kutoa ajira kwa hatua hii ya awali ya ujenzi wa reli kwa (standard gauge), kwa maeneo yote reli itakapopita basi watu wa maeneo yale wasiachwe nyuma, wachukuliwe na kupewa ajira kwa mujibu wa taratibu na sheria kama zinavyosema. Haitapendeza kuona vijana wanatoka maeneo tofauti kuja kufanya kazi katika eneo ambalo nalo lina vijana wasiokuwa na ajira. Mradi huu uwe chachu na mfano kwa miradi mingine hata na nchi jirani ziweze kuiga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari yetu hasa ya Dar es Salaam imekuwa lango kuu na tegemeo kwa nchi mbalimbali zilizotuzunguka. Naipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa mageuzi makubwa ya kimkakati katika kuiboresha bandari yetu hii pia na bandari nyingine zilizopo ndani ya nchi yetu. Bandari ni chanzo kizuri cha mapato kama tu kikitumiwa vizuri na kwa uadilifu mkubwa. Hivyo basi hatua hizi zilizochukuliwa ziwe endelevu ili ziendelee kuleta tija kwa Taifa letu

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto ya kuamini na kuzikubali bandari kavu ila bandari kavu kama tukizipa kipaumbele zitakuwa na msaada mkubwa sana. Hapa nazungumzia bandari kavu za pembezoni mwa miji kama Jimboni kwangu Kibaha Vijijini tumetenga maeneo maalum kwa ajili ya bandari kavu na kama mpango huu ukifanikiwa ina maana utapunguza msongamano ambao uko mjini. Mfano niliwahi kuishauri Serikali humu humu Bungeni kuhusu suala la bandari kavu iliyopo Kwala, bandari hii iwe maalum kwa kuegesha magari yote (used), kwa maana kuziondoa yard za kuuzia magari (used) ambazo zimezagaa kila kona Jijini Dar es Salaam na hivyo kuwepo sehemu maalum ya mtu akitaka magari (used) anajua wapi pa kwenda. Hili limefanyika katika nchi nyingi sana zilizoendelea kama Dubai na kadhalika huwezi kukuta kila kona ya mji kuna yard ya kuuzia magari. Hizi yard zimekuwa zikiharibu mandhari ya miji yetu na uchafuzi wa mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hilo pia la bandari kavu kuwepo na upatikanaji wa spea tofauti tofauti za magari pamoja na mashine mbalimbali. Hiyo itapelekea kuondokana na maeneo ya mijini kutapakaa hovyo maduka ya spea kama ilivyo hivi sasa katika Mtaa wa Shauri Moyo. Hatua hii ikikamilika watu watajua wakitaka magari yaliyotumika yote ama spea zote basi wanakwenda Kwala Kibaha Vijijini na kufanya manunuzi. Itasaidia kuwa na sehemu moja tu ambayo utapata hitaji lako ama gari au spea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili Serikali tayari imeshaonesha nia kwa kutenga maeneo kama ilivyo jimboni kwangu, kilichobaki ni utolewaji wa elimu na uhamasishaji kwa sekta binafsi kuziona fursa hizi na kuzifanyia kazi. Hatua hii ikishakamilika, Serikali itapata fursa ya kuanzisha njia ya treni kutoka Dar es Salaam mpaka Kibaha ili kuwarahisishia wananchi watakaokuwa wakienda katika bandari kavu hiyo na Serikali kupata fedha za uendeshaji. Vilevile Mkoa wa Pwani hivi sasa umekuwa na watu wengi sana, kupatikana kwa usafiri wa treni hiyo kutawasaidia watu wengi sana na kutatua changamoto ya usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya teknolojia yamekuwa yakikua siku hadi siku na Taifa hatuwezi kukwepa ukuaji huo. Ndio maana takwimu za watumiaji wa mawasiliano zimezidi kukua siku hadi siku. Serikali imejaribu sana na inaendelea kujitahidi kuimarisha miundombinu yake na kuwasisitiza wadau wa mawasiliano pia kuzidi kuongeza jitihada mahsusi kwa ajili ya kuleta tija. Leo tunaona Serikali imezitaka kampuni zote za simu za mikono kutoa hisa kwa wananchi na wao kuwa ni wamojawapo wa wamiliki wa haya makampuni lakini bado kuna changamoto katika hili kwani uhamasishaji wa kununua hisa hizo umebaki kwa makampuni yenyewe na si Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali nayo kutilia mkazo juu ya kuhamasisha wananchi ili kuleta nguvu na imani kubwa kwa wananchi wetu. Vilevile naishauri Serikali kuzidi kuchukua hatua stahiki kwa wale wote wanaokiuka sheria na taratibu zilizowekwa kisheria ili kuzifanya sekta hizi kufanya kazi zake kwa kufuata taratibu, sheria na misingi iliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini si kwa umuhimu, naipongeza Serikali kwa juhudi ilizozifanya na inazoendelea kuzifanya kwa shirika letu la ndege. Shirika hili lina historia yake kubwa sana lakini hapa miaka ya karibuni historia hii ilitaka kufutika lakini sasa tuna ndege zetu na nyingine zimeagizwa zinakuja muda wowote. Hatua hii ni ya kujivunia sana na ya kihistoria. Ushirikiano na makubaliano waliyokubaliana kati ya nchi mbili za Ethiopia na Tanzania katika nyaja mbalimbali hususani ya ushirikiano wa mashirika yetu haya ya ndege ni hatua nzuri ukizingatia wenzetu shirika lao ni kubwa na lina historia ndefu. Hatua hizi zote si za kubezwa kwani zitasaidia kuliimarisha shirika letu la ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kwa unyenyekevu mkubwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufika mahali hapa nami kuchangia hoja hii muhimu iliyoko mbele yetu leo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kama kiongozi wa nchi kwa namna anavyoliongoza Taifa letu katika kutuwekea misingi imara. Hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu inatuonesha mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na makadirio ya mapato na matumizi ya fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2018/2019, hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoainishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuendelea kupambana katika vita dhidi ya rushwa nchini kwetu, hali ilivyo hivi sasa ni ya kuridhisha tofauti na hapo awali, kama taarifa inavyosema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 2017 hadi Machi, 2018, jumla ya majalada 325 yalifanyiwa uchunguzi na TAKUKURU na kuwasilishwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ambapo 214 kati ya hayo yalipata kibali cha kuwafikisha watuhumiwa mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ukilinganisha kwa idadi ya kesi zilizopelekwa mahakamani na kesi zilizoamuliwa na kwa idadi ya watuhumiwa waliokutwa na hatia, naweza sema bado tunahitaji kuongeza nguvu zaidi ili kuweza kufikia kiwango ambacho kitawafanya wapenda rushwa kuiogopa rushwa na kujikita zaidi katika maadili mema katika utekelezaji wa kazi za kila siku za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali adhabu katika makosa ya rushwa, watu wanapokutwa na hatia kisheria ya rushwa basi adhabu iwe kali ili iwe fundisho kwa watu wengine. Hata hivyo, naipongeza Serikali kupitia TAKUKURU kwa kufuatilia miradi ya maendeleo na kuhakikisha fedha za umma hazipotei na kutumika ipasavyo kama zilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vita dhidi ya madawa ya kulevya imekuwa kwa kiwango cha juu sana kipindi hiki kupitia mamlaka ya kudhibiti na kupambana na madawa ya kulevya na tumekuwa tukishuhudia taarifa mbalimbali za kukamatwa watuhumiwa mbalimbali na baadhi ya wengine hata kujaribu kutoroka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyowahi kuchangia katika Mabunge yaliyopita, vita ya kupambambana na madawa ya kulevya siyo nyepesi, ni vita ngumu sana inayohitaji kuwawezesha kwa namna ya hali ya juu sana Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Madawa ya Kulevya, maana watu wanaohusika na biashara hii wana uwezo mkubwa kifedha na wana njia nyingi sana wanazoweza kuzitumia ili tu kufanikisha jambo lao. Hivyo basi ni wajibu wa Serikali kuendelea na kuongeza nguvu katika vita hii iwe endelevu na kukomesha kabisa mtandao huu hapa nchini kwetu ili kuwanusuru vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko ya Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Madawa ya Kulevya, 2015 yaliyofanyika yameleta tija kubwa sana. Niishauri tu Serikali pale itakapoona kuna hoja ya kufanya marekebisho mengine, basi sisi Wabunge tuko tayari kushiriki kwa lengo la kuhakikisha madawa ya kulevya yanakuwa historia katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naipongeza Serikali kwa kuendelea kuimarisha na kuongeza huduma ya watumiaji wa dawa za kulevya kwa kutumia methadone katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Temeke na Mwananyamala, ila naiomba Serikali kuongeza juhudi zaidi ili huduma hii iweze kufika mbali zaidi kwa waathirika wa dawa za kulevya wako kila kona ya nchi yetu kuanzia vijijini na maeneo yote ambayo hupatikanaji wa huduma hii ni mgumu, kufanya hivyo kutasaidia sana kuokoa maisha ya vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali katika kuimarisha ulinzi na usalama katika mipaka yetu, hii inatuweka katika usalama zaidi katika kipindi hiki ambacho dunia inapita mapito mbalimbali ya kitahadhari. Vilevile naipongeza kwa kuliwezesha jeshi la polisi kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na majeshi yake mengine, bila kulisahau Jeshi la Wananchi kupitia Wizara ya Ulinzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie afya, kwanza niipongeze Serikali kwa kuboresha huduma mbalimbali za kiafya kwa kuanzia na utoaji wa chanjo nchi nzima. Upatikanaji wa dawa, vifaa na vifaa tiba kwa kuongeza bajeti, upatikanaji wa tiba za kibingwa mfano upandikizaji wa figo, vifaa vya kuongeza usikivu katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili, upasuaji kwa kutumia tundu dogo na kufungua kifua katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo uboreshaji wa miundombinu ya kutolea huduma za afya katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road kwa kuwezesha dawa kupatikana kwa wakati na muda wa kupata huduma ya mionzi kupungua, haya na mengine mengi ni baadhi tu ya maboresho katika Sekta ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kila kwenye kupiga hatua hapakosi kasoro mbalimbali, kama ilivyo katika sekta ya hii ya afya kuna changamoto mbalimbali ambazo Serikali haina budi kukabiliana nazo kwa kuzidi kuipa bajeti ya kutosha Wizara ya Afya na kuhakikisha huduma muhimu zinapatikana nchi nzima na kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya maji nchini imekuwa kubwa sana, Wabunge humu ndani lazima tunakabiliana na changamoto hiyo, ingawa Serikali imeendelea kuweka nguvu kubwa katika sekta ya maji, lakini bado suala la upatikanaji wa maji sehemu mbalimbali za nchi hasa vijijini imekuwa changamoto kubwa sana. Kujenga na kupanua miradi mbalimbali ya maji vijijini itasaidia sana kukabiliana na changamoto hiyo, miradi 71 iliyokamilika bado ni idadi ndogo sana ukilinganisha na miradi inayoendelea kutekelezwa takribani miradi 366.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali kuweka sekta ya maji katika vipaumbele vyake kwani inawagusa watu wetu wa hali duni hasa vijijini ndiyo wanaohangaika kukesha kusaka maji. Naipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazoendelea nazo katika mipango yake ya kuhakikisha kwa mwaka huu 2018/2019 kukamilisha miradi yake ya maji ipatayo 387 kwenye halmashauri mbalimbali nchini na pia kuanza miradi mipya ya maji vijijini, ni jambo jema lazima tulisemee kwa namna ya kupongeza na kuipa moyo Serikali kwa kuonesha inatambua changamoto hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuziboresha bandari zetu nchi nzima ili kuziwezesha katika hali ya kufanya kazi kwa ufanisi, hasa bandari yetu ya Dar es Salam kuiweka katika ushindani mkubwa na kuiwezesha kupata meli nyingi kuja kushusha mizigo hapa na kuendelea kupokea watumishi kutoka nchi jirani kuitumia bandari yetu, uboreshaji huu ni katika Gati namba moja (1) mpaka saba
(7) kuongeza upana wa lango la kuingilia meli na eneo la kugeuzia meli, sambamba na kuboresha mtandao wa reli bandarini pamoja na kujenga gati maalum la kuhudumia meli zinazoshusha magari, hizi ni hatua nzuri, endelevu kwa manufaa ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya Serikali kuja na mpango wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini ni mpango mzuri sana ambao umeweka mgawanyiko wa kimajukumu ,kwani sasa wananchi wa vijiji wamepata wakala wao ambao utakuwa unashughulika na miradi ya barabara za vijijini. Tuseme tu ukweli, wananchi wa vijijini wamekuwa wakisahaulika sana kwa kutokutupiwa jicho la upendeleo, miundombinu imekuwa ni mibovu sana hasa kwa hapa nazungumzia barabara, ambazo zimekuwa hazipitiki na ukiangalia wananchi hawa ndio wazalishaji wa mazao mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwa mpango huu basi barabara nyingi za vijijini sasa zitakarabatiwa na kuwapa unafuu wananchi wetu. Hapohapo naipongeza Serikali kwa kuanza utekelezaji wa ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge) itakayokuwa na urefu wa kilometa 1,219, hadi sasa ujenzi wa kipande cha kutoka Dar es Salam hadi Morogoro kilometa 300 umeanza na unatarajia kukamilika Novemba, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kuna mradi mwingine mkubwa ambao umezinduliwa hivi karibuni wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi bandari ya Tanga. Bomba la mafuta hilo la kusafirishia mafuta ghafi litakuwa na urefu wa kilometa 1,445; kati ya hizo kilometa 1,115 zitajengwa nchini Tanzania. Mradi utakuwa na manufaa kwetu sisi kama nchi na wenzetu wa Uganda, hizi ni hatua za Awamu hii ya Tano kwa maendeleo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sekta ya Elimu ni sekta muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu, tumekuwa tukiona taarifa mbalimbali zikizungumzia sekta hii na Serikali kuchukua hatua mbalimbali pia katika kutatua changamoto ya elimu, lakini lazima Serikali ikaangalia kwa jicho pana zaidi sekta hii ya elimu ili iweze kuendana na dhana nzima ya viwanda ya Serikali hii ya Awamu ya Tano ikiongozwa na Mheshimiwa Dokta John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bila kuja na matokeo chanya yenye tija juu ya mustakabali wa elimu yetu, basi itatuwia vigumu sana kufika malengo ya Tanzania ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda kutumia nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kufika mahali hapa nami niweze kuchangia hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ya mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Spika, kama inavyojieleza, hotuba hii inakwenda kutatua changamoto mbalimbali na kutekeleza miradi ya kimaendeleo inayogusa sekta husika za ujenzi, uchukuzi na mawasiliano. Aidha, inakwenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoainishwa. Pia nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa kuandaa hotuba nzuri yenye malengo chanya.

Mheshimiwa Spika, napenda kuanza kuchangia kwa kuipongeza Serikali katika jitihada zake za kuendelea kuhakikisha nchi yetu inakua na barabra nzuri zinazopitika wakati wote. Lengo kuu la Serikali ni kuunganisha mikoa yote kwa barabara za lami ili kuimarisha na kurahisisha mawasiliano ya usafiri na usafirishaji wa watu, bidhaa na mazao mbalimbali. Ni jambo la kujivunia sana kwani hadi kufikia Februari 2019, jumla ya kilomita 266.78 za barabara kuu za mikoa zimekamilika na kilomita 392.2 zinaendelea kujengwa kwa kiwango cha lami. Vilevile katika jitihada zilezile Serikali imekamilisha ujenzi wa madaraja matano katika Mto Lukuledi (Lindi), Mara (Mara), Sibiti (Singida), Momba (Rukwa na Songwe) na Mlalakuwa (Dar es Salaam) na ujenzi wa madaraja 8 unaendelea katika sehemu mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa miradi hii, utatoa fursa mbalimbali kwa wananchi kupata ajira pamoja na kupata soko kwa bidhaa na mazao yao. Aidha, utasaidia sana kuvutia wawekezaji kuja kuwekeza nchini ikizingatiwa miundombinu yetu ni mizuri.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, bado naendelea kuipongeza Serikali kwa kuendelea kutekeleza ujenzi wa miradi ya barabra inayolenga kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi. Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa barabara kuwezesha mradi wa kuzalisha umeme wa Stigler’s Gorge kwa kiwango cha changarawe kutoka Ubena Zomozi mpaka Selous kilomita 177.6 na ukarabati wa barabara ya kutoka Kibiti - Mloka – Selous – Mpenda (Km 370), Makutano – Natta – Magumu - Liliondo (Km 239) na Loliondo - Lumecha (Km 464). Haya yote kwa ujumla yamefanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi yenye viongozi imara wenye kutekeleza yale yote yaliyomo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM, ikiongozwa na Rais wetu shupavu na mpenda maendeleo.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa ujenzi wa awamu ya kwanza wa reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro kwa asilimia 42.8 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Novemba, 2019. Hali kadhalika, ujenzi wa awamu ya pili wa reli hiyo ya kisasa kutoka Morogoro - Makutupora Jijini Dodoma umefikia asilimia 6.07. Hadi sasa mradi kutoka Dar es Salaam - Makutupora umeshaajiri wafanyakazi wazawa wapatao 6,335 sawa na asilimia 90 ya wafanyakazi wote. Ni jambo la kupongezwa kwani limezalisha ajira kwa watu wetu na kuna faida kubwa mradi husika utakapokamilika.

Mheshimiwa Spika, sambamba na ujenzi wa reli mpya ya kisasa, Serikali katika mwaka 2018/2019 imeendelea na kazi ya kuboresha, kujenga na kukarabati miundombinu ya reli ya kati kwa kuondoa reli zote nyepesi na kuweka reli mpya zenye uzani wa paundi 80 kwa yadi kati ya stesheni ya Dar es Salaam na Isaka. Aidha, kazi ya ukarabati wa reli ya Tanga- Arusha imekamilika kwa sehemu ya Tanga – Same (Km 199). Hata hivyo, katika mwaka 2019/2020, Serikali itaendelea na kazi ya ujenzi wa reli ya kisasa, ukarabati wa ujenzi wa reli ya kati na nyingine ikiwemo ya Tanga – Arusha ili kuimarisha huduma za usafirishaji na biashara kwa ujumla. Miradi hii inatekelezwa chini ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi ikiongozwa na Rais wetu anayetekeleza Ilani ya Chama.

Mheshimiwa Spika, tumeendelea kuwa na changamoto ya msongamano katika Jiji letu la Dar es Salaam na imejitokeza pia katika baadhi ya miji, lakini Serikali imefanya na inaendelea kufanya jitihada kubwa kutekeleza miradi ya kuondoa msongamano wa magari kwenye Jiji la Dar es Salaam ili kurahisisha usafiri na usafirishaji na kuchochea shughuli za kiuchumi kwani Jiji hili lina bandari kuu ambayo huchangia pato la nchi kwa kiasi kikubwa. Hivyo, jitihada hizi zinafanyika kulingana na hali halisi iliyopo.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa kukamilisha ujenzi wa mradi wa barabara ya juu ya Mfugale na miradi mingine inayoendelea. Miradi ambayo ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji ni ujenzi wa barabara za juu kwenye makutano ya Ubungo (Ubungo Interchange), upanuzi wa barabara ya Kimara Mwisho - Kiluvya (Km 19.2) kutoka njia mbili kuwa nane. Katika mradi huu upanuzi wa hii barabara ya njia nane, naishauri Serikali mradi huu uweze kuishia mizani ya Vigwaza. Kwa kufanya hivyo kutasaidia sana kupunguza msongamano ambao sasa pia umeanza kujitokeza katika Mkoa wetu wa Pwani hasa Kibaha.

Mheshimiwa Spika, aidha, pongezi hizi pia zinakwenda katika mradi mpya wa daraja jipya la Salender na miundombinu ya mabasi yaendayo haraka awamu ya II na III. Hata hivyo, katika mradi wa mabasi yaendayo haraka kwa awamu ya kwanza kumejitokeza changamoto mbalimbali na za muda mrefu ambazo wananchi wamekuwa wakizilalamikia za uhaba wa mabasi, abiria kujaa kwa wingi na kwa muda mrefu kwenye vituo vya mabasi hayo. Pia changamoto ya uwepo wa baadhi ya mabasi ya express, mabasi haya ya express hayana tija kwa kuwa miundombinu ya mabasi haya yenyewe yanajitosheleza kufika kwa haraka. Kero ya mabasi haya ni pale yanapoacha abiria vituoni ili hali kuna uhitaji, athari zake ni abiria kuzidi kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni kama ifuatavyo, mabasi yote ya express yarudishwe katika hali ya kawaida ili kukidhi mahitaji kwa sababu hivi sasa mradi unakabiliwa na uhaba wa mabasi. Kufanya hivyo, kutasaidia kupunguza mlundikano wa abiria katika vituo vya mabasi. Aidha, naishauri Serikali katika mradi huu wa mabasi yaendayo haraka awamu ya pili ufike mpaka Kibaha. Kuleta mradi mpaka Kibaha kutarahisisha usafiri kwa wananchi kwani mkoa wetu sasa umekua hasa Kibaha tunaongezeko kubwa la watu wanaokuja kuishi na kufanya shughuli zao mbalimbali, pia ni eneo ambalo linakua kwa kiwango kikubwa katika ukuaji wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kuanzisha treni ya moja kwa moja kutoka Posta hadi Mlandizi. Uwepo wa treni hii utakuwa na tija kwani treni inabeba abiria wengi kwa wakati mmoja ukilinganisha na usafiri mwingine. Mfano tumeona mabasi yetu yanayotumika katika mradi wa mabasi yaendayo haraka, mabasi haya ni ya gharama kubwa, utunzaji wake pia ni wa gharama pamoja na vipuri vyake. Hali hiyo inapelekea mabasi haya yanapoharibika kuchukua muda mrefu kukarabatiwa na hivyo kupunguza ufanisi wa mradi huu lakini tutakapokuja na treni itatusaidia sana kupunguza adha hii ya usafiri.

Mheshimiwa Spika, aidha katika mradi huo wa treni, naishauri Serikali kwenye kila kituo treni itakaposimama kujengwe maegesho ya magari ya kulipia ili wananchi wanapotoka katika maeneo yao wanaacha magari yao hapo na kupanda treni. Hii itasaidia kuingiza kipato katika maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine inayotukabili wana Kibaha Vijijini ni kukosekana kwa mawasiliano ya uhakika. Kuna maeneo hakuna minara na hivyo kuifanya dhana nzima ya uchumi wa viwanda kuwa ngumu, kwani mawasiliano ya simu ni muhimu, yanakwenda sawia na dhana nzima ya uchumi wa viwanda. Maeneo hayo ni Ruvu Station, Ruvu kwa Dosa, Kipangege, Miande, Dutuni, Madege, Lukunga, Videte, Boko Mpiji, Kwala, Mperamumbi Msua na Waya.

Mheshimiwa Spika, hapana shaka yoyote juu ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya barabara kama nilivyokwishapongeza hapo awali. Katika mwaka 2019/2020, Serikali itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kwa mikoa ambayo haijaunganishwa na barabara kuu za lami. Kibaha Vijijini tuna changamoto kubwa ya miundombinu ya barabara, tuna bandari kavu Kwala ambayo kwa kiasi kikubwa inakwenda kuleta mapinduzi makubwa sana lakini barabara zake haziridhishi. Naiomba Serikali kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Vigwaza- Kwala kwani ikiwa katika kiwango cha lami itavutia wawekezaji kuja kuwekeza eneo hili na kurahisisha uchukuaji wa mizigo.

Mheshimiwa Spika, aidha, tuna changamoto ya barabara za Chalinze – Magindu, tunaomba ijengwe kwa kiwango cha lami. Hata hivyo, kuna mradi mkubwa wa ujenzi wa miundombinu ya reli ya kisasa SGR lakini barabara hii inayoelekea katika mradi huo kuanzia Kongowe – Soga ilipo karakana tunaomba ijengwe kwa kiwango cha lami. Kwa sasa maeneo yale kutokana na mradi huu shughuli za kiuchumi zimekua kwa kiasi kikubwa, kujengwa njia hii kwa kiwango cha lami kutazidisha kasi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Makofia- Mlandizi - Mzenga ni ya muda mrefu. Barabara hii imeongelewa hapa Bungeni tangu Mbunge wa kwanza hadi awamu yangu nimekuwa nikiisema hapa Bungeni ijengwe kwa kiwango cha lami lakini hadi leo hatujapata majibu ya kuridhisha ama utekelezaji. Barabara hii ina umuhimu mkubwa kwani inaunganisha Majimbo takribani manne ya Bagamoyo, Mkuranga, Kibaha Vijijini na Kibaha Mji. Kwa umuhimu wake, hakika barabara hii inahitaji ijengwe kwa kiwango cha lami hasa ikizingatiwa kila Mbunge aliyewahi kuongoza Jimbo hili amewahi kuizungumzia.

Mheshimiwa Spika, wakati wa kipindi cha kampeni mgombea wa nafasi ya Urais wakati huo ambaye hivi sasa ndio Rais wetu, alituahidi wana Kibaha Vijijini kujengewa barabara kwa kiwango cha lami yenye urefu wa kilomita 10. Hii ni ahadi ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ambapo mpaka leo hii tumebakiza takribani mwaka na nusu wa kumaliza kipindi cha miaka mitano haijatekelezwa. Ni aibu kwa Chama kwani tukirudi tena kuomba ridhaa kwa wananchi hawa tutawaambia nini? Ni vema ahadi zote za Mheshimiwa Rais alizoahidi kutekelezwa kwa wakati kabla hajamaliza muda wake. Namuomba Mheshimiwa Waziri wakati wa majumuisho atupatie majibu ya hoja hizi ili nasi wana Kibaha Vijijini tuwe na matumaini.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuwa mahali hapa na kupata nafsi hii muhimu kabisa ya kuchangia Hotuba ya Bajeti ya Serikali ya mwaka 2019/2020. Hotuba hii inakwenda kuhitimisha bajeti kuu ya Serikali katika mipango mbalimbali na mikakati, aidha, bajeti hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoelekeza. Halikadhalika nitumie fursa hii kwa mara nyingine tena kuipongeza Serikali kwa kuandaa hotuba nzuri, inayokwenda kutupatia mwelekeo wenye tija kwa maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kutoa pongezi nyingi kwa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa ya kusimamia wanyonge kupinga ufisadi kuhakikisha maliasili zote zinainufaisha nchi na watu wake ili kuleta maendeleo kwa Taifa, katika bajeti ya mwaka 2018/2019, Serikali imetuambia ilitarajia kupata jumla ya shilingi trilioni 32.48 kutoka katika vyanzo vyote vya ndani na nje. Aidha, mchanganuo wa mapato yaliyopatikana hadi Aprili, 2019 ikilinganishwa na lengo la kipindi hicho ni kama Serikali ilivyoainisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapato yasiyo ya kodi yalifikia shilingi trilioni 2.04 sawa na asilimia 122 ya lengo. Mapato yasiyo ya kodi yalivuka lengo kutokana na kuimarika kwa matumizi ya teknolojia katika ukusanyaji wa maduhuli kwenye taasisi za Serikali kupitia mfumo wa kielektroniki wa Serikali wa ukusanyaji wa mapato (Government electronic payment Gateway –GEPG); mapato ya Halmashauri yalifikia shilingi bilioni 529.25, sawa na asilimia 72 ya lengo; misaada na mikopo nafuu kutoka kwa Washirika wa Maendeleo ilifikia shilingi trilioni 1.70 sawa na asilimia 86 ya lengo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo ya ndani ikijumuisha mikopo ya kulipia dhamana za Serikali zilizoiva ilifikia shilingi trilioni 3.3, sawa na asilimia 57.4 ya lengo; na mikopo ya masharti ya kibiashara ya nje ilifikia shilingi bilioni 692.3, hizi ni hatua nzuri zilizofikiwa na Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuhakikisha kila lengo lililopangwa linatimia kwa wakati na kulifanya Taifa lisonge mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika Serikali imetueleza namna ilivyoshindwa kwa baadhi ya maeneo kutofikiwa kwa malengo ya mapato ya kodi kulitokana na sababu mbalimbali zikiwemo ugumu wa kutoza kodi sekta isiyo rasmi, kuendelea kuwepo kwa upotevu wa mapato kunakosababishwa na tatizo la magendo hususani kupitia bandari bubu kwenye mwambao mrefu wa Bahari ya Hindi na mwamko mdogo wa wananchi kudai risiti za kieletroniki wanapofanya manunuzi au baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu kutotoa risiti wanapofanya mauzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuishauri Serikali katika changamoto hii, kutotoa risiti ama kwa wananchi kutokudai risiti ni jambo ambalo linahitaji muda kuweza kulitatua. Kwanza elimu ya kutosha itolewe kwa wananchi ili wajue ni wajibu wao kudai risiti, wasipodai risiti wanapoteza mapato ya Serikali na hivyo kupelekea kwa baadhi ya miradi ya maendeleo kutokukamilika hasa katika huduma za kijamii ambazo zinawagusa wananchi moja kwa moja. Vilevile Serikali ianzishe sasa kutoka elimu ya wajibu wa kulipa kodi tangu shule za msingi ili kutengeneza kizazi kijacho chenye kutambua umuhimu wa ulipaji kodi, msingi huu utasaidia sana kwa mustakabali wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha Watumishi wa TRA wana wajibu wa kutoa elimu kwa walipa kodi na kutokutumia vitisho pale wanapokusanya kodi. Imejengeka hali ya uoga na vitisho kati ya mlipakodi na mkusanya kodi kwa baadhi ya watumishi hawa kujenga mianya ya rushwa na kupelekea kwa baadhi ya wafanyabiashara kufunga hata biashara zao kwa kuona kodi wanazodaiwa ni kubwa kuzidi mitaji ya biashara zao. Vilevile naishauri Serikali kuangalia uwezekano wa kuzirasimisha bandari bubu ili sasa zitambulike na kukomesha uhalifu unaofanyika huko, kuzirasimisha bandari hizo kutasaidia Serikali kupata kodi ambayo sasa wanaikosa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto ya muda mrefu ya malimbikizo ya madai mbalimbali ya Wazabuni, Watumishi wa Serikali na kadhalika kuidai Serikali. Changamoto hiyo pia imewakumba baadhi ya watumishi wa Serikali Jimboni Kibaha Vijijini hasa katika Sekta ya Elimu kuwa na madai ya muda mrefu, lakini Mheshimiwa Waziri ametuambia Serikali imeendelea kuhakiki na kulipa madeni ya wazabuni, makandarasi na watumishi ambapo hadi Mei, 2019 kiasi cha shilingi bilioni 598.4 kimelipwa kati ya bajeti iliyotengwa ya shilingi bilioni 600.0 kwa mwaka 2018/2019. Kati ya kiasi kilicholipwa shilingi bilioni 300.5 ni kwa ajili ya Wakandarasi, shilingi bilioni 232.9 ni kwa ajili ya watoa huduma na shilingi bilioni 65.0 ni kwa ajili ya Watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha tumeelezwa kuwa, Serikali imelipa malimbikizo ya kimshahara ya Watumishi 790 waliostaafu kabla hawajalipwa, ambapo hadi Aprili, 2019, jumla ya shilingi bilioni 3.10 zililipwa, ni hatua nzuri sana, lakini bado changamoto ipo ukilinganisha na hali halisi, malimbikizo haya yanapolipwa ama kwa wazabuni, watumishi basi yanakwenda kusaidia sana katika kukuza uchumi wa watu kwani fedha hizo zinakwenda kuingia kwenye mzunguko na hivyo kusaidia hali ya uchumi wa chini, kati kuwa katika hali nafuu. Naishauri Serikali kuongeza kiwango cha kulipa malimbikizo hayo ili kuleta nafuu kwa wadai na wategemezi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara wanaouza kwa rejereja bidhaa mbalimbali baada ya kufanikisha kuzinunua kwa wazalishaji wakubwa kwa maana ya viwanda wamekuwa wakitozwa kodi, ni jambo jema sana kwani kodi ndio msingi wa maendeleo katika Taifa lolote lile duniani, lakini sasa naomba kuishauri Serikali kuanza kutumia aina tofauti ya ukusanyaji wa mapato ambayo kwa kiasi kikubwa itawaondolea wenzetu wa TRA usumbufu wanaoupata katika kukusanya kodi kwa wafanyabiashara wa mwisho, kwa maana wale wanaouza kwa rejareja, Serikali iweke mfumo maalum wa TRA wa kukusanya mapato kwa pamoja hasa katika vyanzo vya uzalishaji wa bidhaa mbalimbali, mfano Viwanda vya Mabati, Nondo, Saruji, Vinywaji mbalimbali, Viwanda vya Sukari na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huo uwe unakata kodi zote mpaka ya mfanyabiashara wa mwisho kwa maana ya wale wanaofanya kwa rejareja, kwa maana hiyo mfanyabiashara huyu wa rejareja anapokwenda kuchukua bidhaa kwa mzalishaji mkubwa (Kiwanda) anauziwa bidhaa anazohitaji kwa bei ambayo itakuwa imejumuisha kodi zote pamoja na kodi ambayo kwa sasa wafanyabiashara wa mwisho wanakatwa. Hatua hii itakwenda kusaidia zaidi watu wa TRA kwa kupata kodi yao kwa uhakika bila kusumbuana kama ilivyo sasa, tunaona namna ukusanyaji wa kodi kwa wafanyabiashara wa mwisho (rejareja) unavyosuasua kwa namna ya elimu ama wengine kutokutoa risiti kwa kila bidhaa wanayoiuza. Vilevile hatua hii itapunguza nguvu kubwa inayotumia Serikali katika kukusanya kodi kwa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu mwingine kwa Serikali, ni kuanzisha mikoa ya kikodi kwa Sekta nzima ya Maliasili na Utalii, mikoa hiyo ya kikodi kazi yake ni kukusanya kodi zote husika zinazotokana na maliasili na utalii, mfano katika sekta nzima ya utalii, kuna mahoteli, vivutio vya utalii na mambo mengine mbalimbali yanayohusiana na sekta nzima ya utalii, Serikali ikifanya hivyo itakwenda kusaidia sana ukusanyaji wa kodi katika sekta nzima ya utalii na kuepusha ukwepaji wowote ambao kwa namna moja au nyingine kwa baadhi ya watu wasiokuwa waaminifu wamekuwa wakikwepa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wetu wa kukusanya kodi ni mzuri sana, napenda kuipongeza tena Serikali kwa jitihada inazofanya katika kukusanya kodi, lakini tuna changamoto moja na muda mrefu ambayo imekuwa ikilalamikiwa na Watanzania walio wengi, ni tozo kubwa za kodi zinazotozwa bandari kwa vifaa mbalimbali, mfano, vyombo kama magari, bei ya kununulia nje ya nchi kama Dubai, Japan na kwingineko ni kiasi cha wastani, lakini ukileta hapa nchini, tozo ya kodi ya kutolea gari hiyo inakuwa mara tatu na bei ya chombo halisi, haileti maana hasa ukizingatia bei ya chombo husika iko wazi na inajulikana, najiuliza kwa nini tozo inakuwa kubwa kuliko bei halisi ya manunuzi? Naishauri Serikali kuanza utozaji mkubwa wa tozo za kodi kwa bidhaa ambazo zinazalishwa hapa nchini kwa maana viwanda vyake vipo hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo kuagiza nje ya nchi bidhaa zinazozalishwa nchini ni kuua viwanda vya ndani, kufanya hivyo kutasaidia sana kuviinua viwanda vyetu vya ndani, aidha kwa bidhaa zozote ambazo hazizalishwi hapa nchini, basi Serikali naiomba ichukue ushauri wangu wa kupunguza kodi ili sasa Watanzania waweze kumudu kuagiza vitu mbalimbali, hasa magari kwani ndio tozo zake zimekuwa zikilalamikiwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na kukua kwa miji mbalimbali hapa nchini kwetu, hali hiyo imetupata pia watu wa Kibaha Vijijini, kwani sasa mji unazidi kukua kwa kasi sana na huduma mbalimbali muhimu zinapatikana, idara mbalimbali nazo zinapatikana, mfano Idara ya Maji, tuna ofisi ya Halmashauri pamoja na Jeshi letu la Polisi kwa kituo chetu kupandishwa hadhi, naiomba Serikali sasa kutokana na hayo yote niliyoyataja na mengine mengi yenye kutupa hadhi wana Kibaha Vijijini kuwa na sifa zote, Serikali sasa ni wakati wa kuja kufungua Ofisi za TRA, Kibaha Vijijini, kufunguliwa kwa Ofisi ya TRA kutasaidia kwa kiasi kikubwa kusogea kwa huduma hiyo karibu na wananchi, na pia kutasaidia kwa Serikali kukusanya kodi zake kwa urahisi na kugundua changamoto mbalimbali na kuzifanyia kazi kwa uboreshaji zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza Serikali kwa hatua iliyochukua ya kufuta ada hiyo, ilikuwa kero kubwa kwa wananchi ililinganishwa na hali halisi ya uhaba wa maji na changamoto mbalimbali katika sekta ya maji ambazo ni za muda mrefu. Changamoto hizo zimepelekea wananchi kwa gharama zao wenyewe kuamua kujichimbia visima vyao ili kupata maji kwa matumizi ya nyumbani, lakini wakakumbana na kikwazo cha kulipia kodi, kikwazo hicho sasa kimeondolewa, pongezi tena kwa Serikali, hivyo nawasihi wananchi mbalimbali wenye uwezo kuendelea kuchimba visima kwa kufuata taratibu zilizopo kisheria na kujipatia maji. Hata hivyo, nazishauri Bodi za Maji za Mabonde kuendelea kufuatilia visima vyote ili kuwa na idadi kamili na kuepuka uchimbaji holela unaoweza kujitokeza kwa namna yoyote ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii ya kipekee kabisa kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha na mimi kuwepo mahali hapa na kuchangia hotuba hii ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu 2020/2021 iliyopo mbele yetu. Hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM kama ilivyoainishwa. Napenda kuipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na watalaam mbalimbali kwa kuandaa hotuba nzuri itakayokwenda kuleta mapinduzi makubwa katika nyanja mbalimbali za kimaendeleo.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii pia kwa kuanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri anayoifanya kumsaidia Mheshimiwa Rais wetu, sisi sote ni mashahidi, tumeona Mheshimiwa Waziri Mkuu akiwa katika maeneo mbalimbali kuhakikisha shughuli mbalimbali za kimaendeleo zinakwenda vizuri bila kusuasua, tumeshuhudia usimamiaji mzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015/2020 ukifanywa na Mheshimiwa Waziri Mkuu, ni hatua nzuri na ya kujivunia sana tukiwa sisi wanaCCM, kwani tuliahidi kuwaletea maendeleo wananchi wetu bila kubagua.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano tumeshuhudia mafanikio makubwa katika kuimarisha miundombinu, huduma za kiuchumi na kijamii, utawala bora, mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi pamoja na kuhamasisha uwekezaji nchini kwetu, kuvutia wawekezaji mbalimbali kuja kuwekeza na kuzalisha ajira.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa awamu ya tano kwa uongozi wake mzuri na kuhakikisha utekelezaji wa Ilani ya CCM 2015/2020 unakwenda vizuri. Aidha napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na Serikali kwa ujumla kwa kuendelea kupambana na janga la virusi vya corona (COVID-19), ikumbukwe janga hili ni la kimataifa kama WHO walivyokwishatangaza hapo awali. Janga hili linaendelea kusumbua na kuathiri watu wetu, idadi ya wagonjwa imekua ikiongezeka na hivi karibuni imethibitishwa kuwa mgonjwa mmoja aliyekuwa na virusi hivi na kulazwa katika treatment centre iliyopo karibu na Hospitali ya Mloganzila amefariki dunia. Ni kipindi kigumu sana tunachopitia kulingana na mazingira yetu, lakini ni wajibu wetu kuendelea kushirikiana na kutoa elimu kwa watu wetu juu ya kujikinga na kuchukua tahadhali mbalimbali juu ya ugonjwa huu.

Mheshimiwa Spika, hakika katika kipindi hiki cha janga hili la virusi vya corona (COVID-19) ni vema Serikali ikaangalia ni njia gani ya kukabiliana na janga hili hasa namna ya kuepusha maambukizi mapya kwa wananchi, mazingira yetu yanatofautiana sana na nchi za wenzetu hivyo hatupaswi kuyafanya yale ambayo wenzetu wameyafanya kulingana na mazingira yao, naishauri Serikali kuona umuhimu wa kutenga fedha za kutosha ili kukabiliana na janga hili, hii itasaidia kuweza kukabiliana na aina yoyote itakayojitokeza katika kipindi hiki hatarishi, kwani Tanzania ni moja ya nchi ambazo zina muingiliano mkubwa wa watu, mikusanyiko masokoni bado inaendelea, katika vyombo vyetu vya usafiri bado kuna mrundikano wa watu na baadhi ya maeneo mengine watu wameendelea kukusanyika, maradhi haya hatuwezi yapuuzia, kuwalinda watu wetu ni wajibu wetu. Hata hivyo naipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali ilizochukua baada ya janga hili kutokea, kusitisha mbio za mwenge wa uhuru, kusitisha michezo yote nchini, kusitisha shughuli zote za elimu kuanzia elimu ya awali hadi vyuo vikuu, kusitisha semina, makongamano na mikutano yote ya hadhara, ni maamuzi ya msingi kulingana na aina ya ugonjwa unavyoambukiza.

Naiomba Serikali iendelee kutoa elimu kila wakati katika vyombo vyote vya habari, kuweka matangazo mbalimbali mitaani ili wananchi wapate kujua namna ya kujikinga na janga hili.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kujitahidi kutengeneza fursa mbalimbali za ajira kwa kuendelea kuweka mifumo mizuri ya uwekezaji hasa katika viwanda, ni jambo jema na la kupongezwa, lakini bado tuna changamoto kubwa sana ya ajira kwa vijana wetu, kwa taarifa ya Shirika la Kazi Duniani ya mwelekeo wa ajira kwa vijana ulimwenguni (Grobal Employment Trend for Youth) inaonesha kuwa tatizo la ajira kwa vijana Tanzania wenye elimu kuanzia sekondari na kuendelea ni kubwa kuliko wale wenye elimu ya kiwango cha chini. Aidha, Watanzania wenye elimu za chini wamepata ajira lakini ajira zao ni duni ama kipato cha chini na za mazingira hatarishi kama sehemu mojawapo ya kuwatumikisha kwa kuwa uelewa wao juu ya masuala ya sheria na taratibu za kazi ni mdogo.

Mheshimiwa Spika, lazima tukubali kuwa kilichotufikisha hapa ni aina ya elimu tunayoipata kutoka mashuleni. Hatua ya kwanza ya kulitatua tatizo hili ni kugusa mitaala yetu kwanza, bado ipo kikoloni ndio maana kila kijana anawaza kuajiriwa zaidi kuliko kujiajiri na hili sio kosa lao, yaani hakuna kitu tunachokiogopa kama mitaala yetu ya elimu kuibadilisha ili iendane na mazingira yetu ya sasa ili itusaidie kukabiliana na hili tatizo la ajira kwa vijana.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tunajifunza mambo mengi shuleni ambayo hayana uhusiano wa moja kwa moja na mazingira yetu. Niliwahi kusema kuwa kwa nini mfano tusikubali kuingiza masomo ya ufundi kwenye shule zetu zote za sekondari kutegemeana na mazingira shule ilipo? Cha kushangaza hata zile shule zinazotoa fani za ufundi kwa sasa zipo taabani, hata tukienda kwenye shule hizo tukaulize wangapi wanasomea masomo hayo ya ufundi tutakuta hakuna. Tabaka hili la ukosefu wa ajira kwa vijana ni kubwa sana na kila mwaka idadi inazidi kuongezeka, hii ni nguvu kazi kubwa ambayo ni wajibu wa Serikali kuiwekea mipango mizuri ya ajira ili iweze kuzalisha, vijana kukosa ajira kuna athari zake kubwa.

Naiomba Serikali ije na mpango mzuri zaidi wa kuwasaidia vijana wetu katika kujiajiri na kuajiriwa, Serikali iweze kuajiri vijana wenye uwezo na kuwatengenezea fursa vijana wengine katika ajira binafsi hasa katika kilimo, nchi yetu ina ardhi kubwa sana hivyo tukiwekeza hasa kwenye kilimo kwa vijana wetu tutapata faida kubwa, kwanza ajira yenyewe kwa vijana, kuingiza kipato na Serikali kupata kodi ya mazao, uzalishaji wa chakula utaongezeka na kupelekea Taifa kuwa na chakula cha kutosha. Lakini tukiendelea kusema vijana wajiajiri na hatujawahi kujiuliza wanajiajirije? Hiyo mikopo wanaipataje? Sote tunajua masharti magumu ya benki zetu hapa nchini, benki hawatoi fedha bila kuwa na asset ya kuweka kama bond, hawa vijana wana asset gani? Ni kijana yupi mwenye hati ya nyumba au kiwanja au chochote anachoweza kukiweka kama bond ili apate mkopo?

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto zote nilizotangulia kuzisema na kushauri, lakini naipongeza tena Serikali kwa kuweza kutambua umuhimu wa kundi hili la vijana, kama fursa muhimu na kwa maendeleo ya Taifa, naipongeza Serikali kwa kuendelea na uboreshaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana.

Katika mwaka 2019/2020 Mfuko wa Taifa wa Maendeleo ya Vijana umetoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 3.2 ambapo vikundi 586 vyenye jumla ya vijana 4,222 kutoka katika Halmashauri 155 walipata mikopo hiyo. Hata hivyo naishauri Serikali kuwaendeleza wabunifu mbalimbali katika vifaa mbalimbali walivyobuni ili viweze kulisaidia Taifa letu, na sisi tuwe na vifaa vilivyobuniwa hapa kwetu, hili pia litasaidia kuongeza chachu kwa vijana wetu kuwa wabunifu zaidi.

Mheshimiwa Spika, tuna changamoto pia inayowakabili wenzetu wenye matatizo ya ulemavu, hawa wanapaswa kuendelezwa kulingana na matatizo waliyokuwa nayo, ni wajibu wa Serikali kuhakikisha watu wenye ulemavu wanaendelezwa katika fani mbalimbali ili waweze kujiajiri na si kuwaona baadhi wakiwatumia huko mitaani kuomba omba misaada, hii haileti taswira nzuri kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyojua uwekezaji ni njia pekee inayoleta maendeleo na kuzalisha ajira, tukiwa na wawekezaji wengi hasa katika sekta ya viwanda wataleta tija kubwa na faida kwa wananchi, ni wajibu wa Serikali kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji ili kuwavutia wawekezaji wengi zaidi. Hata hivyo naipongeza Serikali kwa kuendelea kuratibu na kusimamia shughuli za kuhamasisha na kufanikisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuvutia mitaji, teknolojia na ujuzi ambao ni chachu ya maendeleo katika sekta mbalimbali.

Aidha, tumeambiwa Serikali yetu imeendelea kufanya tafiti za kisekta (investment sectoral profiles) ili kubaini hali halisi ya ukuaji, mnyororo wa thamani, fursa zilizopo na changamoto za kisekta kwa lengo la kutoa mapendekezo ya maboresho katika sekta husika, hii itasaidia sana katika kurekebisha baadhi ya maeneo yenye changamoto. Katika hatua za awali tumeona tafiti hizo zimefanyika katika maeneo ya mbolea na kemikali, mifugo na mazao yake, pamba, uchakataji wa mazao ya kilimo kama vile korosho, michikichi na parachichi, nafaka na mbegu za mafuta. Halikadhalika matokeo ya tafiti hizo yameendelea kutumika katika kunadi fursa mbalimbali za uwekezaji ndani na nje ya nchi na kuishauri Serikali kuhusu mikakati na maboresho yanayohitajika katika kuvutia uwekezaji kwenye sekta husika, mwenendo huu ni mzuri na wenye kuleta tija.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa kuandaa mapendekezo ya Bajeti ya mwaka 2020/2021 kwa kuzingatia sera na miongozo ikiwa ni pamoja na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2020/2021. Mpango huu ni wa mwisho katika mfululizo wa mipango ya kila mwaka wa kutekeleza Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano (2016/2017 – 2020/2021) wenye dhima ya kujenga uchumi wa viwanda ili kuchochea mageuzi ya uchumi na maendeleo ya watu wetu. Ni hatua nzuri na ya kuungwa mkono.

Aidha, naipongeza Serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati na kwa gharama nafuu, Serikali imetuambia Mahakama imeendelea kuimarisha huduma kwa kuweka mifumo na taratibu mbalimbali za kuwafikia wananchi katika maeneo yote nchini ili kupunguza mrundikano wa mashauri na kuhakikisha mashauri hayo yanamalizika kwa wakati. Mojawapo ya utaratibu unaotumika ambao ni mzuri na umeleta tija ni kuwatumia Mahakimu wenye mamlaka ya ziada (extended jurisdiction) kusikiliza mashauri ya Mahakama Kuu, ni utaratibu mzuri wenye kufanya sasa Mahakama zetu kutokuwa na mrundikano wa mashauri.

Mheshimiwa Spika, kutokana na jitihada kubwa zinazoendelea kufanywa na Serikali za kujenga uchumi wa viwanda, napenda kuipongeza Serikali kwa kuwezesha jumla ya viwanda vipya zaidi ya 4,000 vimejengwa katika mikoa mbalimbali. Viwanda vilivyojengwa vinazalisha bidhaa za ujenzi, pamoja na viwanda vya kusindika mazao ya kilimo ikiwemo nafaka, matunda, mafuta ya kupikia na bidhaa za ngozi. Ujenzi huu wa viwanda vipya nchini, umechangia kupatikana kwa ajira mpya 482,601 nchi nzima, ni vyema sasa tukaongeza juhudi zaidi ili viwanda viongezeke, wananchi wetu wapate ajira kwa wingi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue fursa hii ya kipekee kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia kuwepo mahali hapa. Vilevile ninamshukuru Mungu kwa kunipa nguvu na nafasi hii na mimi nichangie hotuba hii ya bajeti ya mwaka 2017/2018 ambayo inagusa moja kwa moja maisha ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza Mawaziri pamoja na wataalam wao kwa kuandaa bajeti nzuri yenye kukidhi mahitaji na kutatua kero zilizopo katika sekta nzima ya afya. Bajeti hii inatekeleza Ilani ya chama tawala, Chama cha Mapinduzi. Katika misingi hiyo ilani yetu imezungumzia utekelezaji wa sekta ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Serikali kwa juhudi zake za dhati kabisa katika kuhakikisha huduma za afya zinapatikana kila eneo la nchi yetu, pia kuhakikisha maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto yanazingatiwa kwa mujibu wa sheria zetu na taratibu zilizopo. Kwenye kila jambo lolote la kimaendeleo halikosi changamoto na changamoto hizo yatupasa Serikali kuzichukua kama fursa katika kuhakikisha zinatatuliwa na kuboresha huduma kwa manufaa ya wananchi wetu. Bado tumekuwa na matatizo ya upungufu wa wahudumu wa afya katika zahanati zetu hasa maeneo ya vijijini. Mapungufu haya yamekuwa yakileta kero kwa wananchi wetu kwa kukosa huduma kwa wakati. Kumekuwa pia na upungufu wa madaktari ilhali tunao madaktari wengi waliomaliza vyuo na kufaulu vizuri lakini hawana kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali iajiri watumishi hawa kwa wingi ili waende katika maeneo mbalimbali kuhudumia wananchi. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuwapa ajira madaktari takribani 250 ingawa Wizara hii imesema haina fedha za kuwalipa mishahara, lakini Rais kafanya uthubutu ili wataalam hawa waende kuwahudumia


wananchi. Naishauri Wizara kuchukua hatua madhubuti na kutafuta vyanzo vya fedha ili iweze kuajiri wataalam wa afya wengine. Kufanya hivyo kutasaidia sana kumaliza tatizo hili la muda mrefu la upungufu wa wataalam hawa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sawasawa na hilo, Wizara iweke mkakati wa kujenga nyumba za wataalam wa afya hasa vijijini, mfano katika Jimbo langu la Kibaha Vijijini tuna changamoto kubwa sana ya uhaba wa nyumba za watumishi wa afya na imekuwa kawaida kwa watumishi hawa wakipangiwa kuja katika maeneo ya kwetu, hufika kuripoti na punde wakigundua mazingira siyo rafiki, kwa maana hakuna nyumba basi huondoka kwa kusema wanaenda kuhamisha vitu watarudi, lakini hawatokei tena. Hali hii inarudisha nyuma juhudi tunazochukua kama viongozi katika kujitolea huku Serikali ikilalamika kila siku haina fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya vijijini ndiyo kumeonekana kuna changamoto kubwa ya ukosefu wa nyumba, nafikiri watumishi hawa wanastahili kabisa kukaa sehemu nzuri, Wizara lazima iwe na mkakati wa kujenga nyumba za watumishi hawa wa afya ili kwao iwe motisha na kutoa huduma kwa mazingira yaliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ninaishauri Serikali ihakikishe inaongeza kujenga vituo vya afya ili kuepusha wananchi kutembea umbali mrefu kufuata vituo hivyo vya afya, kwani vimekuwa vikisababisha vifo vya watoto wakati wa kujifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Jimboni kwangu Kibaha Vijijini tumetenga kabisa maeneo ya kujenga vituo hivi, hivyo katika bajeti hii naomba Wizara kupitia Serikali kumaliza changamoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la watoto kuzagaa mitaani nimelisema sana humu Bungeni katika nyakati tofauti na changamoto hii bado ipo. Wizara hii ndiyo wahusika wakuu wa kuchukua hatua na kuhakikisha watoto wote wanakuwa katika vituo maalum siyo kuzagaa mitaani


kuomba omba. Hata hivyo naishauri Serikali kuwachukulia hatua baadhi ya wazazi wa watoto hawa ambao wao ndio wamekuwa wakiwatuma kwenda kuomba na wao wazazi kukaa pembeni. Ni jambo la aibu sana kwa nchi yetu kwani mambo haya yameshapitwa na wakati katika dunia ya leo.

Napenda kugusia pia suala la wazee, natambua uwepo wa vituo vya wazee maeneo mbalimbali hapa nchini, vituo hivi vimekuwa havitengewi bajeti ya kutosha na Serikali na zaidi vituo hivi vimekuwa vikitegemea misaada kutoka kwa jamii. Nafikiri ni wakati sasa Serikali ikachukua hatua kwa kutenga fedha mahsusi kwa ajili ya vituo vyote vya kulelea watoto na wazee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika awamu zote nilizokuwepo humu Bungeni, nimekuwa nikilisemea hili la Kituo cha Afya Mlandizi kupandishwa hadhi, sifa na vigezo tunavyo, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne na Awamu hii ya Tano walitoa ahadi ya kukipandisha hadhi kituo hiki na kuwa hospitali, lakini Awamu ya Nne imepita bila kituo hiki kupandishwa hadhi, sasa tuko Awamu ya Tano naomba ahadi hii itekelezwe, kwani Mheshimiwa Rais akitoa ahadi kinachofuata ni utekelezaji kwa mamlaka husika. Hivyo mimi na wananchi wangu tunashukuru sana katika bajeti hii maombi yetu ya muda mrefu na ahadi za Marais wawili zikitekelezwa.

Mimi kama Mbunge najitahidi sana kujitoa kwa hali na mali katika kuhakikisha majengo na vifaa mbalimbali vinapatikana katika vituo vyetu vya afya, kama sasa kuna ujenzi wa ukuta kwa maana uzio katika kituo cha afya Mlandizi na hizi ni juhudi zangu kama Mbunge, hivyo Serikali ikituunga mkono katika mambo mazuri kama haya basi na sisi viongozi pamoja na wananchi tunafarijika sana na kupata moyo wa kuzidi kujitolea.

Hata hivyo nimeona bajeti ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mwaka 2015/ 2016 hadi shilingi bilioni 251 mwaka 2016/2017, ni jambo jema na la kupongezwa ila rai yangu kwa Serikali ni mamlaka husika


kumekuwa na changamoto za upungufu wa dawa katika vituo vyetu vya afya, zaidi dawa kuchelewa kufika kwa wakati. Naamini kwa ongezeko la bajeti basi changamoto hizo hazitakuwepo tena na kuleta nafuu kwa wananchi kupata dawa kwa wakati na kuwaondolea usumbufu wa kukosa dawa pindi wanapoandikiwa dawa hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kuwepo mahali hapa nami niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara husika kwa mwaka 2017/2018. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuteuliwa katika Wizara hii. Pia nimpongeze Waziri pamoja na wataalam wake kwa kuandaa bajeti nzuri yenye mwelekeo chanya, bajeti hii ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, kwanza niipongeze timu yetu ya Serengeti Boys kwa kuonesha mfano wa kufanya vizuri katika mechi zake zote, hii ni alama tosha na kuikumbusha Serikali kuwa mchezo wowote unahitaji uwekezaji kuanzia chini kwa maana ya kuanzisha vituo vya michezo na kukuza vipaji. Utaratibu huu umekuwa ukifanywa na nchi mbalimbali kama Ulaya, Amerika, Asia na Afrika ingawa sisi hatukuliona jambo hili kwa miaka ya hivi karibuni ukilinganisha na miaka ya nyuma.

Mheshimiwa Spika, michezo hivi sasa ni ajira ambapo imeajiri vijana wengi sana na wamekuwa wakinufaika kama akina Mbwana Samata ambaye anaiwakilisha nchi vizuri sana huko Ulaya. Hivyo, niishauri Serikali bado hatujachelewa tuwekeze katika michezo kwani kuna faida nyingi sana ambazo zitakwenda kutatua changamoto kwa mfano za ajira.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa havifuati taratibu na sheria zilizowekwa. Hata Mheshimiwa Rais aliwahi kulisema hili kuwa baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikivuka mipaka. Habari au uandishi kwa kuzungumzia hapa tunaweza kuona ni vitu vya kawaida tu lakini uandishi wa habari wa aina hasi unaweza kuliingiza Taifa katika machafuko makubwa sana. Mifano iko mingi sana ambayo vyanzo vya machafuko ni vyombo vya habari. Habari zinaenea kwa urahisi sana kuliko kitu chochote na sumu yake ni kali sana.

Mheshimiwa Spika, hivyo, tunahitaji kuwa makini sana na vyombo vyetu vya habari ambavyo habari zake ziko katika malengo hasi, habari zake si za kujenga nchi, wala za kimaendeleo, tuviangalie vyombo ambavyo vinatoa kipaumbele kwa habari binafsi ambazo hazina tija kwa Taifa. Serikali sasa kupitia Wizara ni wakati wa kuchukua hatua kali bila woga wala aibu kwa chombo chochote cha habari ama iwe redio, magazeti au televisheni ambacho kinakiuka taratibu na sheria zilizowekwa. Vinginevyo tukivionea haya na nchi ikaingia katika machafuko kutokana na vyombo vya habari basi ni sisi viongozi ndiyo tutakuwa wa kulaumiwa kwa sababu tulipewa dhamana ya kuvisimamia lakini kwa utashi wetu tukashindwa.

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia utamaduni huwa tunazungumzia tamaduni ya nchi au mahali husika. Sisi kama Taifa tuna tamaduni mbalimbali lakini tamaduni hizi tumekuwa tukiziona tu katika maadhimisho mbalimbali vikundi vikikaribishwa kucheza ngoma na kadhalika lakini hakuna mkakati madhubuti uliowekwa wa kuhakikisha tamaduni zetu zinadumishwa kwa namna yoyote na kuzitangaza. Tamaduni zetu ni fursa kama tukizitumia vizuri kwa sababu wageni watakuja kuziangalia na sisi tumejaliwa kuwa na makabila zaidi ya 100, hivyo tamaduni tunazo nyingi sana. Naishauri Serikali sasa kuchukua hatua katika sekta hii pia ili kuiwezesha kukua na kuleta manufaa kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, juzi Jijini Dar es Salaam wasanii wetu wa Bongo Movie waliandamana na dhumuni lao ni kuzuia filamu za nje kutokuuzwa nchini na kuzipa kipaumbele filamu za kwao. Nina ushauri mzuri kupitia Wizara hii naamini utawafikia. Kuzuia filamu za nje sio utatuzi bali wasanii wetu wanatakiwa kuangalia ni wapi walipokosea mpaka soko lao likashuka. Bila kujua walipokosea na kujirekebisha haitakuwa suluhisho kwao kwani hata wakizuia hizo filamu za nje na zikabaki za kwao tu pia soko halitakuwa zuri.

Mheshimiwa Spika, wananchi wamekuwa wakilalamika sana kuhusu ubora wa filamu za ndani kuanzia kwa waigizaji, vifaa wanavyotumia na matukio katika filamu zao. Ninavyofahamu, filamu haiwezi kutengenezwa kwa miezi miwili halafu ikawa tayari sokoni, ni ngumu kuingia katika ushindani wa soko la filamu hata tu la Afrika Mashariki. Hatuwezi ndugu zangu ni lazima tuishi kwa kujifunza, asiyetaka kujifunza lazima atakuwa na mawazo mgando.

Mheshimiwa Spika, hivyo tuwape elimu vijana wetu wa Bongo Movie kuacha kuharakisha filamu kwa miezi miwili au mitatu kuitoa sokoni huku ubora ukiwa finyu. Hakika wakibadilika watauza kwani hapo nyuma walikuwa wakifanya vizuri katika soko hili hili la filamu. Kama nilivyosema hapo awali ni wakati wao kujiuliza ni wapi walipokosea na kujipanga.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuanza kwa kumshukuru Mungu kwa kunifikisha mahali hapa salama ili nami nichangie hotuba hii muhimu ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ya Mwaka wa Fedha 2018/2019. Naipongeza Wizara pamoja na wataalam wake kwa kuandaa bajeti nzuri. Bajeti hii itatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi katika kuhakikisha nchi yetu inaimarisha ushirikiano na mahusiano mazuri na mataifa mengine duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa juhudi mbalimbali inazochukua katika kuimarisha mahusiano yetu na mataifa mbalimbali duniani, ni hatua nzuri na ya kupongezwa, hatua hiyo italiwezesha Taifa kufaidika na masuala mbalimbali ya kimaendeleo na mataifa hayo. Juhudi hizo zitasaidia pia kulitangaza Taifa letu na kuvitangaza vivutio vyetu na kuvutia watalii, wawekezaji kuja nchini kuangalia fursa mbalimbali tulizokuwa nazo za kiuwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya kufungua ubalozi mpya nchini Israel ni ya kupongezwa. Taifa hilo limepiga hatua kubwa kimaendeleo, uchumi, viwanda na teknolojia. Ubalozi huo utatuweka karibu, kushirikiana katika masuala mbalimbali ya kimaendeleo. Naishauri Serikali kupitia Wizara hii kuwakumbusha Mabalozi wetu wote wanaotuwakilisha katika nchi mbalimbali, kutumia fursa hiyo kuvitangaza vivutio vya kitalii tulivyo navyo na fursa mbalimbali za kiuwekezaji zilizopo nchini, hatua hiyo itasaidia sana kunufaika kama nchi kwa sekta husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Umoja wetu wa Afrika Mashariki unazidi kuimarika na kuleta taswira nzuri ya kimaendeleo. Watu wetu wanaendelea kufaidika na ushirikiano huo kwa kiasi kikubwa, wafanyabiashara wetu wanavuka mipaka na kushirikiana na wenzao katika biashara mbalimbali. Hii ndiyo dhana ya ushirikiano huu ambao una tija kwa kila Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hazikosekani, hivyo naishauri Serikali kuziangalia kwa jicho la pekee changamoto zote na kuzipatia ufumbuzi ambao utaleta malengo chanya kwa mataifa yote wanachama.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha na mimi kufika mahali hapa na kuchangia bajeti hii iliyopo mbele yetu. Bajeti hii inakwenda kutekeleza mipango, miradi mbalimbali ya kimaendeleo, vilevile inakwenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu nzima ya Wizara kwa kuandaa bajeti nzuri yenye mrengo chanya wa kubadilisha sekta nzima ya ujenzi, uchukuzi na mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imekuja na mipango mbalimbali ya kimaendeleo, mipango hiyo ni pamoja na miradi mikubwa ya ujenzi wa reli ya kisasa kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge) yenye urefu wa kilometa 1,219 uendelezwaji wa barabara zikiwemo za juu (flyover) pamoja na kununua meli na vivuko, pia kulifufua shirika letu la ndege na kuliwezesha sasa kuanza kutoa huduma ndani na nje ya mipaka kwa kiwango cha juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pongeza kwa Serikali kwa kuendelea kuboresha mtandao wa barabara nchini, ujenzi wa kilometa 776.45 za barabara kuu kwa kiwango cha lami umekamilika na kilometa 1,760 zikiendelea kujengwa. Vilevile barabara zenye urefu wa kilometa 17,054 zimekarabatiwa, ujenzi wa madaraja mbalimbali kukamilika na mengine kukarabatiwa, hizi ni hatua nzuri zilizofikiwa na Serikali katika kuhakikisha miradi hii inakwenda kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kuja na mpango wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tanzania Rural and Urban Roads Agency-TARURA) mpango huu ni mzuri kwani unakwenda kurahisisha huduma za usafirishaji na kuongeza kasi ya wananchi kujiletea maendeleo, lakini bado tuna changamoto mbalimbali ambazo naishauri Serikali kuzichukua kama fursa na kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Jimboni kwangu na maeneo ambayo mradi wa barabara ya Bagamoyo – Mlandizi - Mzenga umepita hawajalipwa fidia mpaka leo na kukaa kwa muda mrefu bila kuwalipa fidia, hivyo kuwasababishia hasara kwani kiwango wanachotakiwa kulipwa kitakuwa ni kilekile ili miaka inavyozidi kusonga mbele gharama ya vitu inazidi kupanda juu.

Naiomba Serikali hasa katika bajeti hii kuwapa kipaumbele wananchi wangu niliowazungumzia hapo awali walipwe fidia zao na wao waendelee na shughuli zao za kimaendeleo, hata hivyo naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha bajeti yake aje na majibu ya wananchi hawa ili waweze kusikia kauli ya Serikali juu ya lini sasa watalipwa fidia zao?

Mheshimiwa Naibu Spika, Soga kuna mradi mkubwa wa ujenzi wa reli, mradi ule umeleta ajira kwa wananchi wangu na wa maeneo mengine pia, lakini naleta ombi kwa Serikali tunahitaji barabara ya kiwango cha lami kutoka Kongowe - Soga ijengwe kwani kujengwa kwa barabara hiyo kutarahisisha shughuli za usafirishaji na kufikika kwa urahisi kwenda kwenye mradi husika na kuleta maendeleo kwa wananchi. Vilevile barabara ya Bagamoyo - Makofia – Mlandizi - Mzenga zijengwe kwa kiwango cha lami ili kurahisisha shughuli za kibiashara kwani eneo hilo ni muhimu kiuwekezaji na pia naishauri Serikali kujenga bandari ya nchi kavu eneo hilo ili mizigo itakayoshushwa Bandari ya Bagamoyo iweze kuhifadhiwa mahali hapo na kuleta nafuu kwa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ya Kwala, Dutumi na Vigwaza barabara hiyo nayo tunaomba ijengwe kwa kiwango cha lami ili kurahisisha shughuli za kimaendeleo na kuinua uchumi wa maeneo husika. Kama nilivyosema hapo awali kuhusu hizo barabara zina umuhimu sana kwa maendeleo ya Jimbo langu na kwa nchi kwa ujumla na zikikamilika zitasaidia kuleta maendeleo kwa haraka na kuvutia wawekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia mawasiliano ya simu yanavyosaidia katika nyanja mbalimbali katika dunia ya leo, hata hapa nchini kwetu tumeona jinsi mawasiliano ya simu yanavyoleta tija kwa watu wetu na hata kutoa huduma mbalimbali za kifedha kwa kupitia mitandao hiyo ya simu. Hata hivyo, teknolojia hii imeleta pia maendeleo mbalimbali kwa wale watu wanaotumia kwa mrengo chanya. Pongezi ziende kwa Serikali kwani wameendelea kuboresha maeneo mbalimbali, kama kutekeleza Awamu ya Tatu ya Mradi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, hatua hii ni nzuri na imesaidia sana pamoja na ujenzi wa kituo cha kuhifadhia data.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya maeneo Jimboni kwangu wananchi hawana kabisa mawasiliano ya simu, kwa maana hakuna minara maeneo hayo ambayo ingewawezesha wananchi hawa kupata mawasiliano ya simu katika shughuli zao za kila siku, maeneo hayo ni Kata ya Boko - Mpigi, Mkalambati, Kata ya Doga - Kipangege, Misufini, Kata ya Kawawa - Kimara, Makazi Mapya, Makutupora, Msua, Mpelamumbi, Waya; Kata ya Mtongani- Madimia, Kisabi; Kata ya Kikongo- Ngeta, Mkino, Lupungo; Kata ya Ruvu - Kitomondo, Ruvu Station; Kata ya Dutumi - Madege, Dutumi, Muembe Ngozi; Kata ya Gwata - Mguruka, Vinyenze, Ndwati, Kigoda; Kata ya Magindu - Lukenge, Masaki, Miyombo, Lukalasi, Magindu Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua katika mpango wa Serikali kama ulivyoainishwa wa kuendelea na ujenzi wa miundombinu ya kufikisha huduma ya mawasiliano vijijini. Je, maeneo hayo niliyoyaorodhesha hapo juu yatapatiwa mawasiliano katika mwaka huu wa fedha na kama si katika mwaka huu basi naomba kujua ni lini maeneo hayo yatapata mawasiliano na kuondokana na kero hiyo ya muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali katika mradi wa ujenzi wa barabara ya njia sita kutoka Dar es Salaam na kuishia TAMCO ni mpango mzuri wa kimaendeleo, lakini nina ombi na ushauri kwa Serikali yangu sikivu, mradi huu usingeishia tu tamko bali mradi huu ungeendelea mpaka Chalinze na kufika Morogoro kwani uhitaji wa mradi huo kwa maeneo hayo upo na utasaidia sana kuleta maendeleo kwa haraka, kurahisisha shughuli za usafirishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mungu muweza wa yote kwa kuniwezesha kuwepo mahali hapa. Nami niungane na wenzangu kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli hotuba hii imekuja na majibu ya kutatua changamoto mbalimbali zilizopo katika sekta ya habari, utamaduni, sanaa na michezo. Hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi katika nyanja zote muhimu zinazohusika katika Wizara hii, naipongeza Wizara kwa hotuba nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali kwa kuendelea kuhakikisha masuala mazima ya michezo yanakwenda vizuri na kuhakikisha timu zetu za michezo mbalimbali zinashiriki mashindano ya kimataifa na kupata ushindi. Hata hivyo, kuna changamoto mbalimbali katika sekta ya michezo, naomba kuzungumzia uwakilishi wetu katika mchezo wa soka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakika matokeo ya uwakilishi wetu kimataifa katika soka umekuwa si wa kuridhisha kabisa. Timu zetu kuanzia kwenye vilabu na timu ya Taifa tumekuwa ni wasindikizaji katika mashindano ya kimataifa. Serikali imekuwa ikijitahidi sana kuwekeza katika
mpira wa miguu lakini bado tumeshindwa kuwa na matokeo chanya pindi tunapokwenda katika mashindano hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kuja na mkakati kabambe wa kuanzisha shule za mpira wa miguu na michezo mingine kuanzia mashuleni mpaka vyuo vikuu. Hii itatusaidia kupata na kukuza vipaji tangu vijana wetu wakiwa bado wadogo na kupelekea kupata wanamichezo wa michezo mbalimbali ambao sasa watakuja kuwakilisha nchi na kutuletea vikombe mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirikisho letu la Mpira wa Miguu liangaliwe kwa jicho la karibu ili kuondoa dhana ya viongozi wake kuona kwamba ni mahali pa kwenda kujipatia fedha zisizokuwa halali yaani fedha chafu. Wajikite katika masuala ya mpira wa miguu kuhakikisha wananyanyua kiwango cha mpira kwa namna ambayo itatutangaza kama Taifa, lakini siyo kila kukicha ni migogoro tu inatokea kwa kutofautiana kati ya kiongozi na kiongozi na kuacha dhana nzima na malengo ya Shirikisho la Mpira wa Miguu. Serikali kupitia Wizara ichukue hatua kali pale inapoona kuna upungufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufike mahali sasa tuangalie michezo mingine au kitu kingine kitakachotutangaza kimataifa kwa upande wa sanaa, utamaduni au sanaa ya muziki ama inavyoitwa na vijana wetu wa sasa Muziki wa Kizazi Kipya. Tumejionea baadhi ya wasanii wakifanya vizuri kimataifa na kulitangaza jina la nchi yetu Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana hawa wanavyofanya vizuri kimataifa wanaitangaza nchi na kuiwezesha kupata wageni kwani wageni hutaka kuijua zaidi nchi husika baada ya kuona wimbo au msanii husika katika nchi zao akipewa heshima na taasisi mbalimbali. Hata hivyo, tumeshuhudia wasanii wetu wakikosa kuungwa mkono, baadhi ya watu kutokuona yale mazuri yote wanayoyafanya tena kwa juhudi zao wenyewe kulitangaza Taifa na Wizara kuja na kuwafungia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kupitia Wizara wakumbuke kuwa vijana hawa wanatumia nguvu nyingi na gharama kubwa kujitangaza na kulitangaza Taifa. Ni vyema wawe wanakaa nao na kuwashauri, Wizara igeuke kuwa mlezi wa wasanii wetu na siyo kuwa mkandamizaji. Leo wasanii wetu wanapata nafasi ya uwakilishi wa ufunguzi wa Kombe la Dunia kule nchini Russia kwa kwenda kutumbuiza. Mashindano yale ni makubwa duniani, dunia nzima watakuwa wanatazama na watataka kujua msanii huyu anatokea wapi. Wakijua Tanzania watataka kujua Tanzania kuna nini mpaka Shirikisho la Soka Duniani liweze kumchagua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huo ndiyo mwanzo mzuri wa kuanza kupokea wageni kuja nchini kwa shughuli mbalimbali za kiutalii, hata uwekezaji. Je, wasanii wetu kama hawa ambao wanapambana kwa hali na mali na kupata fursa kama hizo tunawaunga mkono kwa kiwango gani? Ni lazima Wizara itambue ni wapi kuna fursa ya nchi kutambulika kisanaa, kimichezo na kadhalika na kuhakikisha inashikamana na wahusika katika kuleta malengo chanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kupitia Wizara kuendelea kuvisimamia vyombo vya habari kwa mujibu wa sheria ili vitekeleze majukumu yao kwa utaratibu uliopangwa, kanuni na maadili ya uandishi wa habari. Kufanya hivyo kutasaidia sana kuwa na vyombo bora vya habari na uhakika wa habari zenyewe kwani tunajua umuhimu wa vyombo vya habari na waandishi wa habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tasnia ya habari inapotumika vizuri katika kutoa habari basi Taifa hubaki salama, lakini pale itakapopotoka na kutoa habari za kichochezi basi Taifa lazima litaingia katika machafuko na amani kutoweka. Wizara iwe inavikumbusha vyombo vya habari wajibu wao ili navyo vitekeleze majukumu yao kwa uhuru na haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuwa hai mpaka leo hii, na kuniwezesha kufika mahali hapo salama na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Bajeti ya Wizara husika ya mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara kwa kuandaa Bajeti nzuri yenye mrengo wa kimaendeleo na uboreshaji wa sekta zote muhimu zinazohusiana na Wizara hii, sekta ya elimu, sayansi na teknolojia. Bajeti hii inakwenda kutekeleza mipango mbalimbali iliyopangwa kufanyika katika Awamu hii ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kuendelea kutoa elimu bure nchi nzima kuanzia shule za awali mpaka kidato cha nne. Hii ni hatua nzuri inayopaswa kupongezwa kwani idadi ya watoto wetu wanaoanza shule imezidi kuongezeka maradufu. Hatua kama hizi zinahitaji kupongezwa na kuishauri Serikali pale panapojitokeza changamoto ili Serikali iweze kuboresha na watoto wetu waweze kupata elimu bora yenye tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna changamoto kubwa sana kwa upande wa walimu wa masomo ya sayansi, aidha, upungufu huu unachangia pia kutokuwa na wanafunzi wa kutosha katika masomo ya sayansi, aidha, upungufu huu utatupelekea kutotimiza ile ndoto ya Tanzania ya viwanda kwani dhana nzima ya viwanda inahusishwa na sayansi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kuendelea kutilia mkazo katika masomo ya sayansi na ikiwezekana kutoa motisha kwa walimu ambao watakwenda kusomea sayansi na wale watakaokuwa wanafundisha masomo hayo, aidha na kwa wanafunzi pia ili kuwafanya wapende masomo ya sayansi kwa upande wa wanafunzi na kwa upande wa walimu motisha hiyo itawafanya kufundisha kwa hamasa kubwa watoto wetu na hivyo kufika lengo la kuzalisha vijana wengi watakaomaliza michepuo ya sayansi na kuja kulisaidia Taifa letu kukuza uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ihakikishe inapeleka walimu wa kutosha hasa maeneo ya vijijini, kwani ndio kuna changamoto kubwa ya upungufu wa walimu na nyumba za kuishi. Aidha, tuna changamoto kubwa ya upungufu wa walimu wa nyumba za kuishi. Aidha, naishauri Serikali kuhakikisha inaongeza matundu ya vyoo katika shule zetu zote nchini na hasa shule za vijijini ndizo zinazokutana na changamoto kubwa za mapungufu hayo kwani hata muamko wa wazazi katika kujitolea na kuchangia kwa hiari masuala ya kujenga matundu ya vyoo, nyumba za walimu na madarasa imekuwa ni mgumu sana kulinganisha na shule za mijini, ambazo nyingi hazina changamoto hizi. Hivyo, ni vema katika bajeti hii hasa ikazingatia masuala muhimu katika kuboresha sekta nzima ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na malalamiko ya muda mrefu kuhusu ubora wa mifumo ya elimu yetu nchini, malalamiko hayo yanapaswa kuchukuliwa kama fursa na Serikali na si ya kuyabeza kwani wadau wa elimu wote ni Watanzania na wanataka maboresho ama mabadiliko yafanyike ili kuokoa sekta nzima ya elimu na mdororo unaoweza kuja kuleta shida hapo siku za mbeleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ikae na wadau wa elimu kuchukua mawazo yao na kusikiliza ushauri unaotolewa na sisi Wabunge na kuufanyia kazi bila kuwa na elimu bora yenye tija, hatuwezi kuwa nchi ya viwanda na tutasababisha watu wetu kuwa watumwa ndani ya nchi yao kwani watakuja wawekezaji kutoka nje na kukosa wataalam kutoka ndani na hivyo kuja na watalaam toka nje kuja kushika nafasi hizo na kuwafanya wazawa kuwa watumwa. Ili kuliepuka hilo Serikali haina budi sasa kuwekeza vya kutosha katika elimu ili kuwa na Taifa bora ni lazima sekta ya elimu iwe imara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakuwa tunajidanganya tukisahau sekta ya elimu na kuzipa kipaumbele sekta nyingine huku tukisema nchi imepiga hatua, ni wajibu wa Serikali kuzipa kipaumbele sekta zote lakini zile zinazobeba mustakabali wa nchi zikaangaliwa kwa upana wake, tukumbuke hakuna hatua nchi inapiga kama watu wake wakiwa wanapata elimu isiyokuwa bora na isiyoendana na viwango vya kimataifa.

Mheshimiwa Spika, jimboni kwangu tuna changamoto nyingi sana katika sekta ya elimu, mimi nikiwa kama mwakilishi wa wananchi na mdau mkubwa wa elimu nimejaribu kutatua baadhi ya changamoto hizo kwa gharama zangu nikishirikisha wadau mbalimbali ili tu wananchi wangu wapate elimu bora, nimeshawahi kutoa vitabu mbalimbali kwa elimu ya msingi na sekondari, kuchangia madawati, ujenzi wa ofisi za walimu, madarasa na matundu ya vyoo na nimekuwa nikifanya hivyo kila mara na pale inapobidi ili kupunguza changamoto hizo pasipo kuisubiria Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda Serikali inapokuja katika jitihada zake za kuleta maendeleo basi ikute sisi kama wadau tumeshaanza kushiriki ili Serikali nayo iweze kumalizia, lakini bado tuna changamoto nyingi ambazo sasa Serikali naiomba ije na majibu ili wananchi wajue zitatatuliwa kipindi gani? Tuna changamoto ya vyumba vya madarasa na kupelekea chumba kimoja kutumiwa na wanafunzi hadi 150 katika shule ya msingi Mtongani, japo changamoto hiyo ipo katika shule zote, lakini kwa shule hiyo tajwa hapo imeelemewa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, tuna changamoto ya samani za ndani katika ofisi za walimu zilizopo, hakuna furniture hivyo kuwafanya walimu wanapokuwa katika majukumu yao ya kila siku kuyafanya katika mazingira magumu sana, na tatizo hilo lipo kwa shule zote, na baadhi ya shule zina upungufu mkubwa wa ofisi za walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo tuna changamoto pia ya nyumba za walimu, walimu wetu Kibaha Vijijini hawana nyumba za kukaa na ikitokea ikawepo basi nyumba moja huwapasa kukaa walimu zaidi ya wawili, hali hiyo sio nzuri kwani huwarudisha nyuma walimu wetu kiutendaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto ya matundu ya vyoo, hali hii huwafanya walimu na wanafunzi kutumia sehemu moja jambo ambalo si utamaduni wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu wanalalamika sana kuhusu stahiki zao ambazo ni za muda mrefu, hali hii ya madai haya huwarudisha nyuma kiutendaji walimu wa jimboni kwangu, tuna changamoto ya upungufu wa walimu mkubwa sana, walimu waliopo ni wachache na hawatoshelezi na kukidhi vigezo, naiomba Serikali kupitia Wizara ije na majibu ya changamoto hizo tajwa wakati wa majumuisho ya Bajeti ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kujua ina mkakata gani kutatua changamoto nilizokwisha zitaja hapo juu ili wananchi wa Kibaha Vijijini wapate elimu bora na walimu pia wawe katika mazingira mazuri na ifike mahali walimu wakisikia wanapelekwa Kibaha Vijijini basi wafurahie na isiwe kama ni adhabu kwani kutakuwa tayari na mazingira rafiki ya kufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyenzi Mungu kwa kuniwezesha kufika mahali hapa na mimi niweze kuchangia hoja hii muhimu iliyopo mbele yetu. Bajeti hii ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa mwaka 2018/2019 inakwenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi katika kutimiza yale yote iliyoyaanisha katika Ilani hasa kukamilisha miradi yote iliyopo katika sekta ya maji na umwagiliaji. Naipongeza Wizara kwa kuandaa bajeti nzuri inayokwenda kuleta mapinduzi makubwa kwa kutatua kero zinazowakumba wananchi wetu hasa katika sekta ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya maji nchini imekuwa kubwa sana, Wabunge wote humu Bungeni tunakabiliana na changamoto hiyo nchi nzima ingawa Serikali imeendelea kuweka nguvu kubwa katika sekta ya maji, lakini bado suala la upatikanaji wa maji sehemu mbalimbali za nchi hasa vijijini imekuwa changamoto kubwa sana, kujenga na kupanua miradi mbalimbali ya maji vijijini itasaidia sana kukabiliana na changamoto hiyo, miradi 71 iliyokamilika bado ni idadi ndogo sana ukilinganisha na miradi inayoendelea kutekelezwa takribani miradi 366.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kuiweka sekta ya maji katika vipaumbele vyake kwani inawagusa watu wetu wa hali duni hasa vijijini ndiyo wanaohangaika kukesha kusaka maji usiku kucha na kuacha kufanya shughuli za kiuchumi na kimaendeleo. Naipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazoendelea nazo katika mipango yake ya kuhakikisha kwa mwaka huu 2018/2019 kukamilisha miradi yake ya maji ipatayo 387 kwenye Halmashauri mbalimbali nchini na pia kuanza miradi mipya ya maji vijijini, ni jambo jema na lazima tulisemee kwa namna ya kupongeza na kuipa moyo Serikali kwa kuonyesha inatambua changamoto hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inajitahidi sana katika kuwaletea maendeleo wananchi wetu kwa kasi ya hali ya juu, lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali katika safari hiyo ya maendeleo. Changamoto hizo zimenigusa mimi pamoja na wananchi wangu wa Kibaha Vijijini, kwa muda mrefu sasa tunaendelea kukabiliana na changamoto hiyo kwa muda mrefu sasa. Miradi ya maji ambayo ndiyo ingewakamua wananchi hawa kwa kupata maji safi nayo haikukamilika kwa wakati na ikizingatiwa chanzo cha maji kipo katika eneo lao na wao wamekuwa walinzi wazuri wa chanzo hicho ili kuepuka uharibifu wa aina yoyote unaoweza kutokea na kuleta athari kwa watumiaji wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wamekuwa wakishuhudia maji yakipita na kwenda maeneo ambayo yamekuwa sugu kwa changamoto ya maji ni Magindu, Gwata, Kipangege, Mwanabwito na Kisabi. Naomba katika bajeti hii kupewa kipaumbele katika sekta ya maji hasa katika miradi ya maji maeneo husika ili iweze kukamilika kwa wakati, na kwenye baadhi ya miradi ambayo ina changamoto ya kusimama kufanya kazi kutokana na kuharibika miundombinu yake basi nayo ipewe kipaumbele kwa kufanyiwa ukarabati wa haraka ili huduma iweze kurejea kwa wananchi, hii itasaidia kwa utekelezaji wa miradi ya maji ili wananchi waondokane na kadhia hiyo ya muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kuja na mkakati kabambe ikishirikiana na Wizara ya Kilimo ambao utakwenda kuanzisha utaratibu maalum wa kutoa elimu kwa wananchi hasa wakulima ili kuondokana na kilimo kilichopitwa na wakati na kuja na kilimo cha kisasa cha umwagiliaji ili kuwawezesha wananchi kuweza kufanya kilimo cha umwagiliaji nchini. Ushirikiano huo wa hizi Wizara mbili utaleta mabadiliko makubwa hasa katika sekta hizi husika. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuchukua fursa hi kumshukuru Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kufika mahali hapa na mimi nichangie hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ya mwaka 2019/2020. Aidha nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na watendaji wa Wizara kwa kuandaa hotuba nzuri, hotuba hii inakwenda kutekeleza ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoainishwa hasa katika masuala mazima ya ulinzi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nianze kwa kuvipongeza vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kwa kufanya kazi kubwa katika kuhakikisha hali ya amani, usalama na utulivu inaimarika. Katika mwaka 2018/2019 Serikali imelitumia Jeshi la Wananchi wa Tanzania kusaidia mamlaka za kiraia katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali kama vile uokoaji wa watu na mali zao pamoja na ujenzi wa Mji wa Serikali katika eneo la Mtumba, Dodoma, hatua nzuri sana na ya kupongezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalipongeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania kwa kuendelea kushiriki kwenye misheni za kulinda amani chini ya mwamvuli wa Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa. Misheni hizo ni MINUSCA huko Jamhuri ya Afrika ya Kati (CAR); MONUSCO Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC); UNAMID nchini Sudan; UNFIL nchini Lebanon; UNISFA huko Abyei na UNMISS nchini Sudan Kusini. Ushiriki wa Jeshi letu pamoja na vyombo vingine vya usalama katika misheni hizo za amani umeendelea kuvipatia uzoefu, kuongeza maarifa na mbinu mbalimbali za kijeshi na kiintelijensia. Aidha, vyombo vyetu vimeendelea kujifunza matumizi ya vifaa vya kisasa na kuanzisha au kuimarisha mahusiano ya kijeshi na nchi nyingine zinazoshiriki kwenye misheni hizo. Jambo zuri ni katika kuimarisha usalama wa raia na mali zao, Serikali imeendelea kudhibiti hali ya ulinzi na usalama nchini kwa kuboresha mazingira ya kuishi askari na kufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuendelea kufanya juhudi kubwa kwa Jeshi letu, katika mwaka 2019/2020 Serikali imeendelea kuimarisha hali ya ulinzi na usalama, kuendelea kutoa fursa za mafunzo kwa vyombo vya ulinzi na usalama, kuvipatia vifaa na zana za kisasa na kuendelea kushirikiana na Jumuiya ya Kimataifa katika kupambana na makosa yanayovuka mipaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyenzi Mungu kwa kuniwezesha kufika mahali hapa na mimi niweze kuchangia hoja hii muhimu iliyopo mbele yetu. Bajeti hii ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa mwaka 2018/2019 inakwenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi katika kutimiza yale yote iliyoyaanisha katika Ilani hasa kukamilisha miradi yote iliyopo katika sekta ya maji na umwagiliaji. Naipongeza Wizara kwa kuandaa bajeti nzuri inayokwenda kuleta mapinduzi makubwa kwa kutatua kero zinazowakumba wananchi wetu hasa katika sekta ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya maji nchini imekuwa kubwa sana, Wabunge wote humu Bungeni tunakabiliana na changamoto hiyo nchi nzima ingawa Serikali imeendelea kuweka nguvu kubwa katika sekta ya maji, lakini bado suala la upatikanaji wa maji sehemu mbalimbali za nchi hasa vijijini imekuwa changamoto kubwa sana, kujenga na kupanua miradi mbalimbali ya maji vijijini itasaidia sana kukabiliana na changamoto hiyo, miradi 71 iliyokamilika bado ni idadi ndogo sana ukilinganisha na miradi inayoendelea kutekelezwa takribani miradi 366.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kuiweka sekta ya maji katika vipaumbele vyake kwani inawagusa watu wetu wa hali duni hasa vijijini ndiyo wanaohangaika kukesha kusaka maji usiku kucha na kuacha kufanya shughuli za kiuchumi na kimaendeleo. Naipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazoendelea nazo katika mipango yake ya kuhakikisha kwa mwaka huu 2018/2019 kukamilisha miradi yake ya maji ipatayo 387 kwenye Halmashauri mbalimbali nchini na pia kuanza miradi mipya ya maji vijijini, ni jambo jema na lazima tulisemee kwa namna ya kupongeza na kuipa moyo Serikali kwa kuonyesha inatambua changamoto hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inajitahidi sana katika kuwaletea maendeleo wananchi wetu kwa kasi ya hali ya juu, lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali katika safari hiyo ya maendeleo. Changamoto hizo zimenigusa mimi pamoja na wananchi wangu wa Kibaha Vijijini, kwa muda mrefu sasa tunaendelea kukabiliana na changamoto hiyo kwa muda mrefu sasa. Miradi ya maji ambayo ndiyo ingewakamua wananchi hawa kwa kupata maji safi nayo haikukamilika kwa wakati na ikizingatiwa chanzo cha maji kipo katika eneo lao na wao wamekuwa walinzi wazuri wa chanzo hicho ili kuepuka uharibifu wa aina yoyote unaoweza kutokea na kuleta athari kwa watumiaji wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wamekuwa wakishuhudia maji yakipita na kwenda maeneo ambayo yamekuwa sugu kwa changamoto ya maji ni Magindu, Gwata, Kipangege, Mwanabwito na Kisabi. Naomba katika bajeti hii kupewa kipaumbele katika sekta ya maji hasa katika miradi ya maji maeneo husika ili iweze kukamilika kwa wakati, na kwenye baadhi ya miradi ambayo ina changamoto ya kusimama kufanya kazi kutokana na kuharibika miundombinu yake basi nayo ipewe kipaumbele kwa kufanyiwa ukarabati wa haraka ili huduma iweze kurejea kwa wananchi, hii itasaidia kwa utekelezaji wa miradi ya maji ili wananchi waondokane na kadhia hiyo ya muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kuja na mkakati kabambe ikishirikiana na Wizara ya Kilimo ambao utakwenda kuanzisha utaratibu maalum wa kutoa elimu kwa wananchi hasa wakulima ili kuondokana na kilimo kilichopitwa na wakati na kuja na kilimo cha kisasa cha umwagiliaji ili kuwawezesha wananchi kuweza kufanya kilimo cha umwagiliaji nchini. Ushirikiano huo wa hizi Wizara mbili utaleta mabadiliko makubwa hasa katika sekta hizi husika. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuwepo mahali hapa nami niweze kuchangia hotuba hii ya Bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya Mwaka 2019/2020. Halikadhalika nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri na watendaji wake wa Wizara kwa kuandaa hotuba nzuri. Hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kwa kuhakikisha sekta nzima ya mifugo na uvuvi inaendelea kuimarika kama ilivyoainishwa.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kuanza kwa kutoa pongezi kubwa kwa Serikali kwa kuendelea kuimarisha sekta ya mifugo na uvuvi kwa kushirikiana na sekta binafsi. Aidha, katika mwaka 2018/2019, Serikali imetuambia ilianzisha dawati la sekta binafsi kwa ajili ya kutatua changamoto zinazowakabili wawekezaji katika sekta za mifugo na uvuvi. Lengo la Serikali ni kuongeza uwekezaji wenye tija utakaowezesha wafugaji na wavuvi kuongeza kipato, kuzalisha malighafi za kutosha za viwanda na kuongeza mchango kwenye Pato la Taifa. Hatua hiyo ni muhimu sana kwa maendeleo chanya ya sekta hii.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo Serikali imeendelea kuhakikisha kwamba sekta ya mifugo na uvuvi inakua na mnyororo mpana wa ongezeko la thamani kwa kutoa kipaumbele katika ujenzi wa viwanda vya kusindika mazao ya mifugo na uvuvi, hatua ambayo inakwenda moja kwa moja kuazimia ile hoja ya kuwa na Tanzania ya Viwanda. Hadi sasa viwanda 99 vya kusindika mazao ya mifugo vimeanzishwa vikiwemo viwanda 17 vya nyama, 76 vya maziwa na sita vya ngozi, hatua ambayo itawasaidia wafugaji na wavuvi hasa kupandisha thamani ya bidhaa zao. Vilevile katika mwaka 2019/2020 Serikali imeendelea kuweka msisitizo katika kuwezesha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika uwekezaji kwenye viwanda, kuimarisha usimamizi wa rasilimali katika ukanda wa uchumi wa bahari na bahari kuu; na kuimarisha miundombinu na kukuza biashara ya mazao ya uvuvi. Aidha naishauri Serikali kutoa elimu kwa wavuvi wetu hasa katika Nyanja ya uvuaji wa Bahari Kuu ili sasa na wao waweze kushiriki kwa namna moja katika kukuza uchumi wa taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Sasa Naomba Nizungumzie Changamoto Zinazotukabili Kibaha Vijijini. Katika Jimbo letu tumeendelea kuwa na migogoro ya wafugaji na wakulima, migogoro hiyo inasababisha kuzorotesha hali ya kiuzalishaji wa kiuchumi kwani muda mwingi wananchi wamekuwa katika migogoro hiyo. Ninaishauri Serikali kuchukua hatua kadhaa zitakazowezesha kupunguza migogoro hiyo, hasa kwa kufanya upimaji wa maeneo yote ya ufugaji wa Kibaha Vijijini ili yajulikane kwa kuweka alama maalum ili kuepusha mwingiliano kati ya wafugaji na wakulima. Aidha Kata ya Kwala kujengwe Ranchi ya kufugia ili wafugaji wakafugie mifugo yao huko. Kufanya hivyo kutapunguza migogoro iliyopo kati ya wafugaji na wakulima ambayo imeendelea kudumu kwa muda mrefu bila kupatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kuanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufika hapa na mimi nashiriki kikao hiki kujadili hotuba hii ya bajeti ya Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka 2018/2019. Hotuba hii imeandaliwa kwa kuzingatia mwelekeo wa nchi hivi sasa kuwa Tanzania ya viwanda. Napenda kuipongeza Wizara kwa kuandaa bajeti nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazoendelea kuzichukua hasa kusimamia na kaulimbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga uchumi wa Taifa unaotegemea viwanda. Kwa maelezo ya Serikali ni kwamba hadi kufikia mwezi Februari 2018 viwanda vipya 3,306 vimeanzishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika viwanda kwa kutoa vivutio vya kodi na visivyo vya kodi kwa wawekezaji mahiri, hii itasaidia kuongeza hamasa kwa wawekezaji wa ndani na wa nje. Hata hivyo naipongeza Serikali kwa kuendeleza na kuboresha miundombinu wezeshi kama vile barabara, reli, bandari, umeme na maji, haya ni maandalizi rafiki na ya kuvutia kwa wawekezaji watakaokuja na kuwekeza. Lakini haikuishia hapo, Serikali imeendelea kuhuisha sera, sheria na kanuni pamoja na kufuatilia utendaji wa viwanda vilivyobinafsishwa na kuchukua hatua stahiki kwa wamiliki walioenda kinyume na mikataba ya mauzo, ni hatua nzuri kwani kuna baadhi ya wawekezaji wasiokuwa waaminifu wamekuwa wakitumia viwanda hivyo vilivyobinafsishwa kwa matumizi tofauti na yale yaliyokusudiwa na Serikali wakati wa sera ya ubinafsishaji. Mpango wa Serikali kwa Mikoa na Halmashauri zote nchini kuwaelekeza kutenga maeneo ya uwekezaji wa viwanda ni mpango mzuri wenye tija na malengo chanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imehakikisha Sekta ya Hifadhi ya Jamii inashiriki kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa viwanda, pamoja na miradi mingine, NSSF na PPF kwa kushirikiana na Jeshi la Magereza wanatekeleza mradi mkubwa wa uzalishaji wa sukari Mkoani Morogoro, ni mpango mzuri na wa kupongezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo hasa la mradi huo ni kuzalisha tani 250,000 za sukari na umeme MV 40, ni mkakati mzuri na wa kupongezwa hasa katika kipindi hiki ambacho Serikali ina mpango wa kufanya nchi yetu kuwa ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa viwanda unaendana hasa na masuala mazima ya kisayansi, hivyo ni budi Serikali kuendelea kufanya tafiti mbalimbali ili kuwezesha kugundua changamoto zilizopo na kukabiliana nazo. Viwanda vina faida kubwa sana kwa maendeleo ya nchi,viwanda hukuza ajira na kuleta maendeleo chanya, nchi kubwa duniani zenye uchumi mkubwa ziliwekeza zaidi katika viwanda na kuweza kuzalisha bidhaa mbalimbali na kuziuza nje ya mipaka yao na hivyo kupata fedha za kigeni. Dhana nzima ya viwanda isibezwe kwani ni mpango wenye malengo mazuri kwa maendeleo ya Taifa letu na ni mpango endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuwa karibu na sekta binafsi, ni jambo la kupongeza kwani sekta binafsi ina mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi nchini, kushirikiana kunaiwezesha Serikali kujua changamoto inazokabiliana nazo sekta binafsi na kuja na suluhisho la kitatuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Wizara kuendelea kuwa walezi wa sekta binafsi na kupokea ushauri ili uchumi wa nchi yetu uweze kuwa endelevu katika ukuaji. Kuna changamoto mbalimbali ambazo sekta binafsi inakutana nazo hasa katika masuala mbalimbali ya kikodi na kadhalika, lakini Wizara inatakiwa kuwa karibu na wadau hawa ili changamoto hizo ziwezekutatuliwa. Nampongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa kukaa na sekta binafsi na kuwapa nafasi ya kuwakilisha kero zao, maoni na ushauri na kwa baadhi ya changamoto kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ina fursa nyingi sana za kiuwekezaji, tuna maeneo mengi ambayo yanavutia kwa wawekezaji, tunahitaji wawekezaji wa ndani na wa nje, ni wajibu wa Wizara kuendelea kuwavutia wawekezaji kuweka mazingira rafiki ili tuweze kupata wawekezaji wengi zaidi kuja kuwekeza katika nyanja mbalimbali na kuzalisha ajira kwa wingi kwa watu wetu. Naishauri Wizara kuendelea kuwachukulia hatua wawekezaji ambao wamekalia baadhi ya maeneo kama viwanda, kuvifunga au kubadilisha matumizi, wanyang’anywe na kupewa wawekezaji wengine wenye nia njema na kuendeleza maeneo husika. Kibaha Vijijini tuna maeneo yaliyopimwa kwa ajili ya uwekezaji, maeneo ni mazuri na ukizingatia Kibaha Vijijini ni mji unaokuwa sasa na hata mazingira ya kiuwekezaji ni mazuri, miundombinu ipo vizuri, hivyo naomba Wizara itupe kipaumbele pale inapopata wawekezaji basi waje Kibaha Vijijini kuwekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha nami kuwepo mahali hapa na kuweza kuchangia hotuba hii ya Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii ya mwaka 2019/2020. Aidha, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na wataalam wa Wizara kwa kuandaa hotuba nzuri, halikadhalika hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa kuhakikisha Sekta nzima ya Maliasili na Utalii inaendelea kuimarika na kuliingizia pato Taifa letu kwa maendeleo ya watu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kuendelea kufanya kazi kubwa ya kiuboreshaji hasa katika Sekta ya Utalii, imeendelea kuimarika na kutoa mchango mkubwa katika ukuaji wa pato la Taifa na kuongeza ajira. Mathalan, idadi ya watalii kuongezeka mara dufu na kupelekea watalii walioingia nchini mwaka 2018 kuongezeka na kufikia watalii milioni 1.49 ikilinganishwa na watalii milioni 1.33 walioingia nchini mwaka 2017. Aidha, hapo hapo pia mapato yatokanayo na utalii yameongezeka na kufikia Dola za Marekani bilioni 2.43 mwaka 2018 ikilinganishwa na Dola za Marekani bilioni 2.19 mwaka 2017, sawa na ongezeko la asilimia 7.13, ni mwanzo mzuri wa kimkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kuendelea na jitihada hizi ili takwimu hizi ziendelee kukua, halikadhalika Serikali imetuambia katika kutangaza vivutio vya utalii, mwaka 2018/2019 Serikali imeanzisha Chaneli ya Utalii (Tanzania Safari Channel) ili kuvutia Watanzania na wageni kutoka Mataifa mbalimbali kutembelea vivutio vyetu. Hatua hii itasaidia sana kuendelea kukuza hali ya kiuchumi kupitia Sekta hii ya Utalii. Kuanzishwa kwa chaneli hii pia, Serikali imetueleza kuwa inaendelea kuimarisha chaneli hiyo kwa kuipatia wataalam, vifaa na vitendea kazi stahiki. Chaneli hii itaendeleza taswira na sifa nzuri ya Tanzania kimataifa sambamba na kuongeza thamani katika mnyororo mzima wa biashara ya utalii nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo pongezi zangu zinakwenda kwa Serikali kuwa na mpango katika mwaka 2019/2020, kuendelea kuimarisha Sekta ya Utalii kwa kuihamasisha na kuiwezesha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika kuendeleza sekta hiyo. Aidha, sanjari na kutangaza utalii, Serikali imeendelea kuimarisha miundombinu ya usafirishaji ikiwemo usafiri wa anga ili kuvutia watalii wengi zaidi nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kuchukua hatua mbalimbali za kimkakati katika kuendelea kupambana na uharibifu wa maliasili kama misitu na kadhalika. Hatua hii imesaidia sana pia hata katika utunzaji wa mazingira yetu na kuepukana na ukame ambao athari zake ni kubwa, kama nchi ikikumbwa na tatizo hilo. Napenda kuishauri Serikali kuendelea na jitihada hizo kimkakati, na kuendelea kupambana na wahalifu wote wanaojaribu kuharibu mazingira yetu kwa kukata miti hovyo, hata hivyo sasa ni wakati wa kutambulisha utalii wa misitu kwani tunayo misitu mingi yenye vivutio kadhaa hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumshukuru Mungu kwa kunifikisha mahali hapa salama ili na mimi nichangie hotuba hii muhimu ya Wizara ya Maliasili na Utalii ya mwaka wa fedha 2018/2019. Ninaipongeza Wizara pamoja na wataalam wake kwa kuandaa bajeti nzuri. Bajeti hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi katika kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya maliasili na utalii.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii pia kwa kuanza kuipongeza Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa jitihada zake za dhati kabisa katika kukuza utalii na kuhakikisha sekta hiyo inaimarika na kuliingizia Taifa pato. Tanzania ni nchi ya pili duniani kwa kuwa na vivutio vya kihistoria, nafasi hiyo ni muhimu sana kwa Taifa na hatuna budi kuitumia ipasavyo kuandaa mikakati mbalimbali ya kimapinduzi katika sekta hii ya utalii ili ilete matokeo chanya.

Mheshimiwa Spika, Tanzania tumebarikiwa kuwa na vivutio hivyo ambavyo havipatikani mahali pengine popote duniani ila ni hapa nchini kwetu. Mikakakati ya kuvitangaza kwa kutumia njia mbalimbali ndiyo njia pekee itakayotusaidia kusikika duniani kote na kupata wageni watakaokuja kutembelea vivutio vyetu na kuliingizia Taifa letu fedha za kigeni pamoja na kutoa ajira kwa watu wetu ambao watahudumu kwa wageni hao. Serikali imejitahidi sana kuliangalia hilo, lakini tukiwa kama sehemu ya Serikali hatuna budi kuishauri pale tunapoona changamoto zinajitokeza hasa ambazo zinarudisha juhudi hizi muhimu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri Serikali kuzidisha matangazo mbalimbali katika maeneo mbalimbali duniani hasa kuvitangaza vivutio vyetu ipasavyo. Tukiwatumia mabalozi wetu katika mataifa mbalimbali wanayotuwakilisha itatusaidia sana kuvitangaza vivutio hivyo na kupata watalii wengi. Aidha, Serikali ije na mkakati wa kuvitangaza vivutio vyote vilivyosahaulika kwani tuna vivutio vya kitalii katika maeneo mbalimbali nchini. Vivutio vya kihistoria ambavyo vimesahaulika sasa ni wakati muafaka kwa Serikali kuvitangaza ili tuweze kupata wageni wa kuvitembelea.

Mheshimiwa Spika, aidha, ninaipongeza Serikali kwa juhudi kubwa ilizoweka na kufanikisha ongezeko la watalii kuja nchini kwetu kwa mwaka 2017 ambapo idadi imefikia milioni 1.33 ikilinganishwa na watalii milioni 1.28 mwaka 2016. Hii imepelekea mapato kuongezeka na kufika dola za Marekani bilioni 2.19 mwaka 2017 ikilinganishwa na dola za Marekani bilioni 2.13 kwa mwaka 2016. Hii ni sawa na ongezeko la asilimia sita, ni hatua muhimu na zinaonesha kuwa sekta hii ya utalii ikijengewa mikakati madhubuti basi italiingizia Taifa letu pato kubwa na kuwezesha maendeleo kuja kwa haraka na hivyo uchumi kukua.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu imebarikiwa kwa kuwa na misitu pamoja na maliasili mbalimbali na Serikali imekuwa ikifanya juhudi kubwa kuyalinda maeneo hayo ya misitu, wanyamapori, malikale, uvuvi, ufugaji nyuki, pamoja na kuhakikisha kwamba rasilimali hizo zinanufaisha vizazi vya sasa na vya baadae.

Napenda kuipongeza Serikali kwa kuchukua hatua za kuimarisha mifumo ya kukusanya mapato katika sekta hizo, kupambana na ujangiri, kuzuia upotevu wa mazao yatokanayo na misitu na kutatua migogoro ya mipaka kati ya hifadhi na vijiji. Hizi ni hatua nzuri na za kupongezwa zinazoendelea kufanywa na Serikali yetu katika mikakati endelevu.

Mheshimiwa Spika, lakini bado kuna changamoto katika maeneo mbalimbali ya uchomwaji wa misitu, uvunaji wa magogo kiholela na kutokutolewa kwa elimu ya kutosha kwa wananchi juu ya upandaji miti.

Mheshimiwa Spika, tukianzia suala zima la uchomaji wa misitu kiholela limepungua kwa kiasi kikubwa, lakini kuna baadhi ya maeneo changamoto bado inajitokeza. Wizara ichukue hatua mbalimbali za kukomesha majanga haya yanapotokea kwani huharibu mazingira hasa kwa baadhi ya maeneo ambayo yana viumbe hai na kwamba hupelekea viumbe hao kuhama.

Mheshimiwa Spika, ni wajibu wa Serikali na taasisi zake za kichunguzi zinazohusika na masuala mbalimbali yanayohusiana na Wizara hii, kuchukua hatua za haraka. Pale kwenye taarifa ama namna yoyote itakayoonesha au kudhihirisha kuna watu wanahujumu sekta yetu hii basi wachukuliwe hatua kali za kisheria na si kuachwa, watu hawa wakiachwa watalipeleka taifa letu katika mgogoro wa kimataifa ama kwa kuharibu mazingira, kuua wanyama wa mwituni na mengineyo yanayofanana na hayo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kufika mahali hapa nami kushiriki katika kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu. Naipongeza Wizara kwa hotuba nzuri yenye mlengo chanya, hotuba hii inakwenda kutekeleza yale yote yaliyoainishwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ili kuleta mapinduzi makubwa ya kiutendaji katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali ilizochukua katika kuliboresha Jeshi letu la Polisi ili lifanye kazi zake kwa uwezo wa hali ya juu kwa kuwapatia vifaa vya kisasa vya mawasiliano na vya kiuchunguzi ili liweze kupambana na ujambazi na matukio mengine ya kihalifu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, napongeza kwa kujenga Kituo cha kisasa cha Mawasiliano (Call Centre) Dar es Salaam ili kuwezesha wananchi kutoa taarifa za matukio mbalimbali kwa urahisi. Haya yote ni maboresho ya hali ya juu kwa Jeshi letu la Polisi ili kuliwezesha kufanya kazi zake pasipo shaka yoyote na kwa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali ilizochukua kuboresha idara nzima ya uhamiaji kwa kuzinduliwa kwa Mradi wa Uhamiaji Mtandaoni (e-Immigration), vilevile kwa kuzinduliwa pasi mpya ya kusafiria ya kielektroniki ya Kimataifa ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhana nzima ya kuzinduliwa kwa pasi hii ni kupunguza vikwazo vya kusafiri mipakani baina ya raia wa nchi wanachama, pia kuimarisha mahusiano na shughuli za kiuchumi baina ya nchi wanachama. Pia naipongeza Serikali kwa kufungua ofisi zaidi za uhamiaji kwenye baadhi ya wilaya lakini naishauri izidi kufungua ofisi zaidi ili kuweza kuwasogezea wananchi huduma karibu na kudhibiti uhamiaji haramu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kumekuwa na changamoto mbalimbali, mfano katika mazoezi muhimu ya kitaifa, kama zoezi la uandikishwaji wa Vitambulisho vya Taifa, Kadi ya Kupigia Kura, kumekuwa na matukio mbalimbali ya baadhi ya wahamiaji wasiokuwa waaminifu kujaribu kujipatia Kadi za Kupigia Kura na Vitambulisho vya Taifa, hali hii inatuonyesha kitu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii inatuonesha kwamba usimamizi wa masuala mazima ya uhamiaji bado kuna changamoto kubwa ya kudhibiti wahamiaji haramu na hii ni hatari kubwa kwa mustakabali wa Taifa letu. Kama hali hii ikiendelea basi nchi yetu inaweza siku kutokea tukatawaliwa na kiongozi ambaye si Mtanzania halisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kujikita zaidi katika kudhibiti uhamiaji haramu na si kufanya kazi kwa mazoea, operesheni za mara kwa mara ziwe zinafanyika nchi nzima ili kuwabaini wahamiaji haramu. Tunapenda watu watakaoishi nchini kwetu kwa kufuata taratibu, sheria na miongozo na si watu wanaotaka kupita njia za panya na kujipatia uhalali wa kujiita Watanzania. Tujifunze kupitia nchi jirani, ama kwa nchi za wenzetu jinsi gani wanavyoweza kudhibiti wahamiaji haramu, Tanzania isiwe shimo la watu kuja na kujiamulia wanavyotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza mazuri yote ya kuiboreshaji yanayoendelea kufanywa na Serikali yetu lakini sina budi kueleza changamoto zinazolikabili jimbo langu na ningependa Waziri atakapokuja kuhitimisha hapa anipe majibu ya changamoto ninazokwenda kuziainisha. Eneo la Kibaha Vijijini ni kubwa kijiografia, gari lililopo la polisi ni moja na ni chakavu haliwezi kabisa kufika maeneo yote ya vijijini na ukizingatia eneo ni kubwa na ukizingatia tena Kibaha Vijijini barabara zake ni mbovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, naomba katika bajeti hii kupatiwa magari zaidi ya polisi ili yaweze kufanya doria na kuhakikisha hali ya kiusalama inazidi kuimarika. Naiomba Serikali kupitia Wizara inieleze hapa ni lini sasa Wizara itatupatia magari hayo ili jeshi letu liweze kufanya kazi zake bila vikwazo vyovyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hakuna makazi ya askari na kuwafanya askari wetu kuishi maeneo tofauti tofauti ambayo ni mbali na eneo lao la kazi. Kuna nyumba ya askari iliyojengwa lakini bado haijakwisha na imekwama kwenye hatua za umaliziaji, nyumba hii ikiisha itasaidia sana askari wetu kuweza kupata makazi bora. Naiomba Serikali kupitia Wizara inieleze ni lini nyumba hii itakamilika na ikizingatiwa imesalia sehemu ya umaliziaji tu. Naiomba Wizara inipe majibu pale Waziri atakapokuja kuhitimisha hotuba yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapofanya uboreshaji wa majeshi yetu lazima tuzingatie na kuyapa kipaumbele pia maeneo yenye changamoto mbalimbali kama maeneo ya vijijini, lazima tuwapatie vitendea kazi vya kutosha kama magari, askari wa kutosha na nyumba za kuishi. Maeneo ya vijijini pakikosekana doria za kutosha na askari ni maeneo ambayo wahalifu huweza kujificha kwa urahisi na kupanga mipango hasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi naishauri Serikali kuyapa jicho la tatu maeneo hayo ili kuwawezesha askari wetu kufanya kazi kwa urahisi ili kuwawezesha kufika maeneo yote yanayowazunguka. Hata hivyo, napenda kuwapongeza askari wote pamoja na wa jimboni kwangu Kibaha Vijijini kwa kuendelea kufanya kazi ingawa kuna mazingira ambayo si rafiki, hii yote wanaonyesha uzalendo wa hali ya juu katika kulitumikia Taifa lao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kutumia fursa hii kumshukuru Mungu, mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kuwepo mahali hapa na kuchangia hotuba hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi katika nyanja mbalimbali za kimaendeleo, uchumi, elimu, barabara, afya na kadhalika. Nichukue pia nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake yote kwa kuandaa hotuba ya bajeti nzuri yenye malengo chanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuipongeza Serikali kupitia Wizara hii kwa kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo na utawala bora Wakuu wa Mikoa yote, mafunzo hayo yametolewa Tanzania Bara. Aidha, Makatibu Tawala wa Mikoa, 26; Wakuu wa Wilaya, 139; Wakurugenzi wa Halmashauri, 185; Maafisa Utumishi,185; Maafisa Mipango, 185; wamepata mafunzo kuhusu majukumu na mipaka ya kazi zao, maadili ya uongozi, utawala bora usimamizi wa sheria, kanuni na miongozo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu ni mzuri na uwe endelevu, kwani mafunzo hayo yamesaidia kuboresha utendaji na kuondoa mwingiliano wa majukumu baina ya viongozi na watendaji. Katika mafunzo hayo, viongozi na watendaji wetu wamekumbushwa wajibu wa kusimamia maendeleo na kutatua kero mbalimbali za wananchi katika maeneo yao ya utawala ili kusaidia kumaliza kama si kupunguza malalamiko ya wananchi ya muda mrefu ambayo yanapelekea kusababisha mabango ya kero zao pindi viongozi wetu wa juu wanapofanya ziara mbalimbali nchini. Napendekeza mpango huu uwe endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inajitahidi sana katika kuwatetea wananchi wetu kwa kasi ya hali ya juu, lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali katika safari hiyo ya maendeleo, changamoto hizo zimenigusa mimi pamoja na wananchi wenzangu wa Kibaha vijijini, kwa muda mrefu sana sasa tunaendelea kupambana na changamoto ya maji, wananchi wangu wanaendelea kukabiliana na changamoto hiyo kwa muda mrefu sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya maji ambayo ndiyo ingewakwamua wananchi hawa kwa kupata maji safi nayo haikamiliki kwa wakati na ikizingatiwa chanzo cha maji kiko katika eneo lao na wao wamekuwa walinzi wazuri wa chanzo hicho ili kuepuka uharibifu wa aina yoyote unaoweza kutokea na kuleta athari kwa watumiaji wa maji, lakini wamekuwa wakishuhudia maji yakipita na kwenda kutumika katika maeneo mengine na wao kuachwa na changamoto ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ambayo yamekuwa sugu kwa changamoto ya maji ni Magindu, Gwata, Kipangenge, Mwanabwito, Kisabi. Naomba katika bajeti hii kupewa kipaumbele katika sekta ya maji hasa katika miradi ya maji ambayo ina changamoto ya kusimama kufanya kazi kutokana na kuharibika vifaa basi nayo ipewe kipaumbele kwa kufanyiwa marekebisho ya haraka, hii itasaidia katika utekelezaji wa miradi ya maji ili wananchi waondokane na kadhia hiyo ya muda mrefu.

Mheshimiwa, Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazoendelea kuzichukua katika suala zima la kutambua ukuaji wa maji na kuchukua tahadhari ili kuepuka yaliyotokea hapo awali katika miji yetu yasijirudie tena, Serikali inatambua ukuaji wa miji na fursa ya kimaendeleo kijamii, kiuchumi kimazingira. Kwa kutambua hilo ndio maana mipango ya matumizi bora ya ardhi ikaandaliwa katika vijiji 1,764 ikilinganishwa na vijiji 12,545 nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu la Kibaha Vijijini tumejiwekea utaratibu wa kuandaa maeneo ili kuepuka matatizo ambayo yamejitokeza katika maeneo mbalimbali nchini kwa kutokutenga maeneo kwa ajili ya shughuli mbalimbali, hivyo basi napenda kuleta ombi kwa Serikali yangu sikivu kupitia Wizara walete na kujenga soko kubwa la kushushia mazao Mlandizi ili kuepusha sasa msongamano ambao upo katika masoko yetu ya mijijini kwa mfano Kariakoo na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mlandizi tuna maeneo makubwa yenye nafasi za kutosha na kupangika hivyo kujenga soko hilo kutasaidia kupunguza msongamano kama nilivyosema hapo awali, lakini si msongamano tu bali pia kutoa fursa ya kuendeleza miji yetu kama Serikali inavyoainisha katika mipango yake, kwani machache ya kuweza kutanua mji huo na ukiangalia mifumo ya mipango miji kwa kiasi kikubwa katika Jiji hili haiko sawa, kwa kuwa ilishakosewa tangu hapo awali.

Mheshimiwa, Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazochukua katika sekta ya afya, hatua hizo ni kama kuratibu na kusimamia hospitali zote za halmashauri, vituo vya afya na zahanati kuhakikisha zinatoa huduma bora kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, changamoto hazikosekani. Katika sekta ya afya, katika jimbo langu baadhi ya maeneo bado changamoto zipo, Vituo vya afya Ruvu, Soga, Magindu, Boko, Gwata, Dutumi, Kata ya Kikongo na Kalangalanga vina changamoto mbalimbali ambazo Wizara kama msimamizi na mratibu wa sekta hii hakuna budi kuzitatua changamoto hizo, kuboresha vituo hivyo vya afya ili viweze kutoa huduma bora kwa wananchi na kupungunza idadi ya vifo vinavyotokana na uduni wa vituo hivyo.

Kuongeza ujenzi wa vituo vya afya kutasaidia sana wananchi wangu kupata huduma kwa wakati pale inapohitajika na kuepuka kutembea kwa muda mrefu kufuata huduma ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ambayo ipo katika Sekta ya Afya jimboni kwangu ni upungufu wa nyumba za watumishi wa vituo vya afya, zilizojengwa na Serikali bado kasi yake hairidhishi. Nashauri Serikali kuongeza kasi ili zikamilike kwa wakati mnamo 30 Juni, 2018 kama ilivyosema. Mpango huu ukikamilika utasaidia kupunguza adha hiyo. Vilevile usambazaji wa dawa na vifaatiba uongezwe kwa kiwango kikubwa ili kurahisisha upatikanaji wa dawa kwa wananchi na vifaa tiba.

Mheshimiwa, Mwenyekiti, Serikali inaendelea kupambana na changamoto katika sekta nzima ya elimu; kutoa elimu bure kuanzia darasa la awali hadi sekondari kuwezeshwe kwani shule nyingi kuwa na madarasa ya awali ni hatua nzuri na inahitaji kupongezwa kwani watoto wetu wanapata elimu wakiwa katika vyumba vya madarasa salama kabisa tofauti na hapo awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, bado changamoto zipo katika sekta ya elimu, baadhi ya maeneo jimboni kwangu tuna changamoto ya matundu ya vyoo, nyumba za Walimu, upungufu wa madarasa, Walimu kulipwa stahiki zao na upungufu wa walimu. Naiomba Serikali kuziangalia changamoto hizi kwa jicho la pekee kwa kuniongezea Walimu, matundu ya vyoo, ujenzi wa nyumba za Walimu na Walimu hawa kulipwa stahiki zao kwa wakati. Mkoa wetu wa Pwani tulikuwa nyuma kielimu ukilinganisha na sasa hivi, changamoto hizi zikiendelea basi zitarudisha juhudi zetu za kuendelea kupandisha kiwango cha elimu jimboni kwangu, matumaini yangu kilio hiki kitapewa kipaumbele kwa maendeleo ya wananchi wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa uendelezaji wa miji ya kimkakati Tanzania ni mpango mzuri kama ulivyoainishwa na Serikali kwa baadhi ya miji, lakini nina ombi;

katika mpango huu pia Halmashauri yetu ya Kibaha Vijijini ingeingizwa katika mpango huu wenye tija kubwa ya kimaendeleo kwa nchi na eneo husika kwani hukuza nyanja nzima ya ukuaji wa fursa mbalimbali za kiuchumi. Hata hivyo, napenda kukumbusha ahadi ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa ya kujenga barabara yenye urefu wa kilometa tano itekelezwe kwani ni muda sasa umepita bila ahadi hiyo kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kumshukuru Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kufika mahali hapa nami kushiriki katika kikao hiki cha bajeti ya Wizara ya Madini ya mwaka 2018/2019. Naipongeza Wizara kwa kuandaa bajeti nzuri itakayokwenda kuboresha sekta hii yenye changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza Serikali kwa kuimarisha usimamizi katika sekta ya madini ili kuwezesha sekta hiyo kuchangia kikamilifu katika uchumi wa nchi, kuongeza mapato ya Serikali na kuzalisha ajira. Hatua zilizochukuliwa na Serikali ni pamoja na kukusanya taarifa za uzalishaji wa madini, kuimarisha ukaguzi wa uzalishaji na mauzo kwenye migodi mikubwa na midogo na kufuatilia ukusanyaji wa maduhuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha naipongeza kwa zoezi la ukaguzi lililowezesha kukamatwa kwa madini yaliyokuwa yakitoroshwa yenye thamani ya Dola za Marekani takribani 898,523 na shilingi milioni 557. Kwa taarifa za Serikali, ni kwamba katika kipindi cha Julai, 2017 hadi Februari, 2018 maduhuli ya Serikali yaliyokusanywa kutoka sekta ya madini yalifikia shilingi bilioni 180.4. Pamoja na mambo mengine, mafanikio hayo yametokana na usimamizi makini katika sekta ya madini na uamuzi wa Serikali kufungua soko la tanzanite nchini. Hatua hizi ni nzuri na ziwe endelevu kwa manufaa ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali imeimarisha soko la madini nchini kwa kuhakikisha kuwa madini yanauzwa kwa ushindani ili kuyaongeza thamani na kulipatia Taifa fedha kwa kupitia kodi. Hata hivyo, itakumbukwa kwamba tarehe 20 Septemba, 2017, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alielekeza ujengwe ukuta katika eneo linalozunguka Mgodi wa Tanzanite uliopo Mererani ili kuimarisha ulinzi na kudhibiti utoroshaji wa madini hayo, ujenzi wa ukuta huo wenye mzunguko wa kilomita 24.5 umekamilika. Nitumie fursa hii pia kuwapongeza viongozi na watendaji wote walioshiriki katika ujenzi huo, kwani umesaidia sasa madini yetu ambayo ni ya pekee kwa kuwa yanapatikana Tanzania tu kuwa salama ukilinganisha na hapo awali.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza pia Serikali kwa kuja na mkakati katika mwaka 2018/2019, kuwa Serikali itaendelea kuwajengea uwezo wazawa ili washiriki kikamilifu katika sekta ya madini, kwani uwezeshaji huo utakwenda sambamba na utoaji mafunzo kwa wachimbaji wadogo kuhusu teknolojia mbadala ya uchenjuaji dhahabu kwa lengo la kupunguza athari za mazingira na maafa katika maeneo ya migodi. Hatua hizi zote hapo juu ni za kujipongeza kwani ni hatua muhimu kwa kuhakikisha sekta hii muhimu inaliingizia pato Taifa na kukuza uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila kwenye mafanikio hapakosi changamoto na changamoto hizo huzichukua kama fursa ili kuboresha maeneo husika. Bado tuna changamoto kubwa hasa kwa wachimbaji wadogo kutopata elimu ya kutosha na kufanya uchimbaji wenye tija na usioleta athari za kimazingira. Wachimbaji hawa wanapaswa kupewa elimu ili uchimbaji wao ulete tija na Serikali iweze kukusanya kodi zake. Naishauri Serikali kuwapa elimu wachimbaji wadogo kama nilivyosema hapo awali katika kuwapa elimu ya teknolojia mbadala ya uchenjuaji dhahabu na pia iwape elimu ya uchimbaji wenye tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali inapaswa sasa kuwaangalia hawa wachimbaji wadogo pindi wanapoagiza vifaa kazi namna ya kuwapunguzia kodi. Kufanya hivyo kutawasaidia kufanya kazi kisasa na kuongeza uzalishaji na kupelekea Serikali kupata kodi yake ipasavyo bila shaka yoyote. Aidha, naishauri Serikali kuendelea kusimamia ipasavyo rasilimali zetu zote katika sekta hii kwani tumeshuhudia mambo mengi ya hovyo yakifanywa na baadhi ya watendaji wetu wasiokuwa waaminifu wakishirikiana na baadhi ya wawekezaji ambao nao sio waaminifu kutudidimiza na kujipatia faida kubwa huku Taifa likiambulia patupu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kumekuwepo na changamoto ya wachimbaji wadogo kuondolewa katika maeneo yao na kutokupewa maeneo mbadala. Ni wajibu wa Serikali kuwalinda wachimbaji wadogo kwani sekta hiyo imetoa ajira kwa watu wetu katika maeneo husika ya machimbo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto ya migogoro baina ya wawekezaji na wachimbaji wadogo, ni vema ikaangaliwa na kutatuliwa kwa wakati ili pande zote mbili husika wakaendelea na majukumu yao ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufika mahali hapa nami kuchangia hoja hii muhimu iliyopo mbele yetu. Vilevile nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa utendaji kazi mzuri katika kuisimamia Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu inatuonyesha mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2019/2020. Hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoanishwa hasa katika kuleta maendeleo kwa wananchi na kukamilisha miradi mbalimbali ya kimaendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite katika kuchangia hotuba hii kwa kuanza na kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi ikiongozwa na Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Mafuguli, kwa kazi nzuri zilizofanywa na zinazoendelea kutekelezwa. Mapendekezo ya bajeti ya Serikali ya mwaka 2019/2020 yamezingatia Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2019/2020 ambao ni wa nne katika mfululizo wa mipango ya kila mwaka ya kutekeleza Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano 2016/2017 – 2020/2021. Dhima ya Mpango huo ni kujenga uchumi wa viwanda ili kuchochea mageuzi ya uchumi na maendeleo ya watu wa Taifa hili. Aidha, mpango huu unatekelezwa sanjari na maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015 – 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi za Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka wa 2015 na zile alizozitoa katika hotuba yake ya kuzindua Bunge hili mwezi Novemba, 2015. Naipongeza Serikali kwa kuendelea kuona vipaumbele vya Mpango wa mwaka 2019/2020 ni kuendelea kuimarisha msingi wa uchumi wa viwanda, kufungamanisha ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu, kuendelea kuboresha mazingira wezeshi kwa uendeshaji wa biashara na uwekezaji na kuimarisha usimamizi wa utekelezaji wa mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango wa Maendeleo na Bajeti ya mwaka 2019/2020, Serikali imeendelea kutekeleza Mradi wa Umeme wa Maji wa Mto Rufiji (Stiegler’s Gorge). Ni jambo kubwa sana na la kupongezwa na si kubezwa kwani tumeshuhudia baadhi ya wapinga maendeleo wakija na hoja mbalimbali za kupinga mpango huu. Aidha, naipongeza Serikali kwa ujenzi wa miundombinu ya reli ya kisasa (SGR), barabara pamoja na kukuza sekta ya anga. Utekelezaji wa miradi hiyo ya miundombinu wezeshi ya kiuchumi una lengo la kufungamanisha ukuaji wa sekta hizo na sekta nyingine hususan za biashara, kilimo na utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokwishatangulia kusema hapo awali kwa kuipongeza Serikali katika miradi yake mbalimbali ya miundombinu na mingineyo, lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali katika miradi hii ambazo mara zote Serikali imezichukulia kama fursa katika kuzitatua. Mradi wa ujenzi wa barabara njia nne (4) ambao kwa hivi sasa unaendelea ni mradi utakaoleta mapinduzi makubwa sana ila napenda kuishauri Serikali mradi huu ujengwe na kufika hadi Ruvu na kuendelea mpaka Mizani Vigwaza. Kwa kufanya hivyo kutasaidia sana kuleta mafanikio makubwa kwa eneo husika ambalo litaongezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Mamlaka za Mji lakini kwa muda mrefu imekosa Mkurugenzi. Naomba katika mwaka huu wa fedha basi Serikali yangu sikivu iweze kutatua changamoto hii kwani kukosekana kwa Mkurugenzi kunazorotesha baadhi ya shughuli za Mamlaka hasa katika kuhudumia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, napenda kuishukuru Serikali kwa kutupatia fedha kiasi cha Sh.2,745,425,524 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Halmashauri. Jengo hili liko katika hatua za mwisho kumalizika. Jengo hili litasaidia sana kupunguza changamoto iliyokuwa inatukabili ya kufuata huduma mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nitoe shukrani zangu za dhati kwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa kwa kutoa mchango wake kiasi cha Sh.1,500,000 aliyotupatia kuchangia ujenzi wa uzio wa Kituo chetu cha Afya Mlandizi. Tunamshukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuwa na dhamira ya kujenga uchumi wa viwanda sambasamba na kuhakikisha upatikanaji wa nishati ya umeme wa kutosha na wa uhakika na nafuu. Kwa kutambua hilo, Serikali yetu inaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya uzalishaji wa umeme yenye lengo la kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi ya uchumi wa kati unaochochewa na ukuaji wa viwanda ifikapo mwaka 2025, hizi ni hatua nzuri na zenye mlengo chanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, hatua kubwa ya uwekaji saini mkataba wa ujenzi wa Mradi wa Bwawa la Kuzalisha Umeme wa MW 2,100 kati ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Kampuni ya JV Arab Contractors & Elsewedy Electric ya Misri ni hatua nzuri na ya kimaendeleo. Mradi huo unaotarajiwa kukamilika 2021/2022 utawezesha ujenzi wa uchumi wa viwanda kwa kuhakikisha upatikanaji wa umeme tena wa bei nafuu na hivyo kukamilisha kivitendo dhana nzima ya mabadiliko na kipaumbele cha kuifanya Tanzania ya viwanda, kwani nishati ya umeme ndio chachu ya kuvutia uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa tu katika sekta hii ya nishati hadi kufikia mwishoni wa Februari, 2019 uwezo wa jumla wa mitambo ya kuzalisha umeme nchini umeongezeka kutoka MW 1,205 mwaka 2015 hadi kufikia MW 1,614 mwaka 2019. Ongezeko hilo limepelekea kuwa na umeme wa ziada wa wastani wa zaidi ya MW 300 ambao utatuwezesha sasa nchi kama nchi kuwa na uhakika wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya Serikali ya kutekeleza kwa mafanikio makubwa Mpango wa Usambazaji wa Umeme Vijijini umekuwa wa mafanikio makubwa sana hasa kwa sisi tunaotoka maeneo ya vijijini kwani kwetu tatizo la ukosefu wa umeme lilikuwa ni changamoto kubwa sana. Kwa ujumla katika mwaka 2018/2019, vijiji 1,782 vimeunganishwa na umeme. Aidha, tangu kuanza kwa usambazaji wa umeme vijijini, tayari vijiji 5,746 vimeunganishwa umeme kati ya vijiji 12,268 vilivyopo nchini, sawa na takribani asilimia 47 ya vijiji vyote. Nalisema hili pasipo shaka yoyote kwani katika vijiji hivyo pia vipo vya Jimboni kwangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia kwenye bajeti hii muhimu. La kwanza kabisa, nichukue fursa hii ya kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa ambayo anaifanya na sisi wote ni mashahidi. Kwa sababu hiyo najikumbusha mbali kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lililopita lile 2010/2015 nilisimama Bungeni hapa na nikasema, kule kwetu mimi ni Mganga wa Kienyeji na nilitabiri kwamba CCM itaendelea kutawala miaka 200. Kwa dalili hizi ambazo naona, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kazi alizozifanya, kwa hiyo, utabiri wangu naona utakamilika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Chama cha Mapinduzi kitaendelea kuongoza kwa miaka mingi. Kuongoza ni kufanya kazi nzuri ambayo wananchi wanaridhika na chama kile ambacho kiko madarakani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo ushahidi wa kazi kubwa ambazo zinafanywa na Mheshimiwa Rais na wasaidizi wake; Mawaziri, kazi kubwa wanazozifanya katika nchi yetu, sisi wote ni mashahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii ya kipekee kumpongeza Mheshimiwa Waziri Jafo kwa kazi kubwa ambayo anaifanya nchi nzima. Sisi ni mashahidi, kila kona anazunguka kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushahidi kidogo tu. Kwenye Jimbo langu naishukuru Serikali nimepata fedha shilingi bilioni1.5 kwa ajili ya hospitali ya Wilaya; pia nimepata fedha shilingi milioni 500 kwa ajili ya Kituo cha Afya. Kituo cha Afya hiki kiko Madindu, lakini nimepata fedha tena shilingi milioni 500 ya Kituo cha Afya cha Mlandizi. Haya yote ni mafanikio ya Serikali hii ya Awamu ya Tano. Ninajivunia, tumepata fedha karibu shilingi bilioni saba kwa ajili ya ujenzi wa soko pale Mlandizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata fedha kwa ajili ya kujenga mabweni shilingi milioni 720. Sasa leo ukisema kwamba Serikali haifanyi kitu napata taabu kidogo. Vile vile tumepata gari la Kituo cha Afya Mlandizi pale, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Ummy kwa kazi kubwa ambayo amefanya tumepata pale gari. Haya yote ni mafanikio makubwa sana katika Halmashauri yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko jambo moja nataka kuzungumzia. Kuna ujenzi wa bandari kavu pale Kwala, nadhani na Mheshimiwa Jafo anafahamu, lakini liko tatizo moja kubwa pale. Tatizo la pale, tukipata barabara ile ya kutoka Vigwaza mpaka Kwala itatusaida sana kule kusukuma mambo kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Waheshimiwa Wabunge wenzangu wameongelea sana suala la TARURA kuhusu kuongezewa bajeti, nami naunga mkono suala hili. Kwenye Jimbo langu kuna tatizo kubwa sana la TARURA kukosa vyombo vya usafiri ili waweze kufanya kazi zao vizuri. Kwa hiyo, namwomba tu Mheshimiwa Jafo, kama mambo yako sawasawa kule atuangalie Jimboni kwetu tupate gari liweze kutusaidia mambo yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalo jambo moja tu la mwisho, kuna suala zima la Walimu. Pale Jimboni kwangu ni tatizo kubwa, Walimu wanalalamika kuhusu kupandishwa madaraja. Kwa hiyo, naomba sana upande huu nao tuweze kuangalia mambo yaende vizuri katika Jimbo pale kwa sababu kama walimu ndiyo wapiga kura wetu na sisi wote tunafahamu, lakini kuna malalamiko makubwa, kwa hiyo, tukiangalia Walimu hawa na yako maeneo mengine wanapandishwa madaraja, lakini sisi bado hatujapanda daraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii ya kipekee tu kuipongeza Halmashauri yangu. Halmashauri yangu mwaka 2018 imekuwa ya kwanza Kitaifa katika ukusanyaji wa mapato. Nawapongeza Madiwani kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kuhakikisha kwamba Halmashauri yetu inaweza kukusanya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeze wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini na mimi mwenyewe kwa kazi kubwa ambazo tunazifanya kwenye Jimbo. Tumeweza kuleta container ya vitabu pale lenye thamani ya dola 250,000; juzi tumeshusha container moja la Vifaa vya Afya pale hospitali shilingi milioni 400; na tunaisaidia hospitali pale kujenga ukuta ule, karibuni milioni 200. Fedha hizo zote zinasaidiwa na nchi na Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mungu, Muumba wa Mbingu na Dunia kwa kuniwezesha nami niweze kuchangia hotuba hii ya Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ya mwaka 2019/2020. Hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoelekeza na kuhakikisha hali ya usalama kwa raia na mali zao unakua wa uhakika. Aidha, nichukue nafasi hii kwa mara nyingine tena kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara hii kwa kuandaa hotuba nzuri.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuipongeza Serikali kwa juhudi kubwa inazoendelea kufanya kwa majeshi yetu ya Polisi, Uhamiaji, Zimamoto pamoja na Magereza. Serikali imeendelea kufanya maboresho mbalimbali hasa kwa Askari wetu, makazi yao pamoja na mambo mengine mazuri yenye tija kubwa hasa katika kuimarisha usalama wa raia na mali zao. Serikali imeendelea kudhibiti hali ya ulinzi na usalama nchini kwa kuboresha mazingira ya kuishi Askari na kufanyia kazi, kutoa huduma bora za kubaini, kutanzua na kudhibiti uhalifu, kudhibiti vitendo vya rushwa ndani ya Jeshi la Polisi pamoja na kushirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi katika kupambana na uhalifu nchini. Haya ni mambo mzuri ya kujivunia hasa katika kipindi hiki. Aidha, hali hii imechangia kupunguza makosa ya kiuhalifu kutoka makosa 37,602 mwaka 2017 hadi kufikia makosa 36,228 mwaka 2018.

Mheshimiwa Spika, halikadhalika kwa upande wa uhamiaji Serikali inatekeleza kwa mafanikio makubwa awamu ya pili ya Mradi wa Uhamiaji Mtandao, ambayo inahusisha utoaji wa huduma ya viza pamoja na vibali vya ukaazi vya kielektroniki. Mradi huu ni wa kisasa kabisa na unaendana kabisa na dunia ya sasa.

Mheshimiwa Spika, vilevile naipongeza Serikali kwa kuzindua mfumo huo hapo mnamo tarehe 26 Novemba, 2018, ambapo sasa unamwezesha mteja kufanya maombi yake kwa njia ya mtandao kama wafanyavyo nchi nyingine zilizoendelea. Hakika mfumo huo, utarahisisha utoaji wa huduma bora za uhamiaji, kuimarisha ulinzi na usalama, kuongeza udhibiti wa wageni wanaoingia nchini, ukusanyaji wa maduhuli ya Seriklai na kuchochea kasi ya maendeleo ya kiuchumi kupitia sekta ya uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kuendelea kuwawezesha Jeshi letu la Zima moto kwa kuwapa vifaa zaidi kama magari ili pindi yanapotokea matukio ya moto iwe rahisi kuyahimili. Pia naishauri Serikali kuangalia upya namna ya kuwatumia wafungwa waliopo Magerezani ili wawe wanazalisha kama alivyowahi kusema Mheshimiwa Rais wetu, wafungwa hawa watumike katika kuzalisha vitu mbalimbali kama mazao. Baadhi wana taaluma zao, pia wazitumie kuleta faida kwa jamii wakiwa huko huko Magerezani.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kutambua umuhimu wa usalama wa raia pamoja na mali zao, kama mdau mkubwa, nimekuwa mstari wa mbele kuhakikisha vituo vya Polisi katika Jimbo langu vinajengwa. Nami kwa kushiriki kwa hali na mali na kuchangia mambo mbalimbali yanayohusu sekta hiyo kama ujenzi wa nyumba za makazi ya Askari wetu, kukarabati gari la Polisi, tumejenga baadhi ya vituo vya Polisi kwa nguvu zetu wenyewe, lakini bado havijakamilika.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali yangu sikivu katika bajeti hii kwa umuhimu wa jambo hili sasa watusaidie kumalizia ujenzi wa vituo hivyo ili vianze kuwahudumia wananchi wangu. Tukifanikiwa kumalizia vituo hivyo, kwa kiasi kikubwa hali ya usalama Jimboni kwangu itazidi kuimarika. Aidha, tuna changamoto ya gari la Polis. Uhitaji wa chombo hicho ni muhimu kwani gari lililopo halitoshelezi kuhudumia Jimbo zima. Tukipatiwa gari litasaidia kufanya doria za mara kwa mara ikizingatiwa Jimbo letu ni kubwa kiutawala.

Mheshimiwa Spika, naleta tena ombi hili kwa Serikali yangu sikivu kutusaidia gari la Polisi katika bajeti hii. Halikadhalika, tumekuwa na migogoro ya wakulima na wafugaji na kupelekea maafa. Nakuomba Mheshimiwa Waziri aje Jimboni kwangu kututembelea na kutatua changamoto iliyopo ambayo inahusisha pia na Jeshi letu la Polisi.

Mheshimiwa Spika, aidha, bado tuna changamoto ya nyumba za Polisi. Namwomba Mheshimiwa Waziri wakati wa majumuisho aweze kutupatia majibu ya maombi yetu na changamoto nilizoziainisha.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha nami kufika mahali hapa na kuchangia Hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ya mwaka 2019/2020. Hotuba hiii inakwenda kutekeleza Ilani a Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoelekeza hususani katika kukuza sekta ya elimu kwa kutoa elimu bure kuanzia darasa la awali hadi kidato cha nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko la udahili kwa wanafunzi wa elimu ya juu na masuala mazima ya teknolojia. Halikadhalika nitumie nafasi hii kwa mara nyingine tena kumpongeza Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali kwa hatua kubwa ilizofikia katika sekta ya elimu, uandikishwaji wa wanafunzi wapya katika mfumo rasmi wa elimu nchini unaonesha kuwa hadi Machi, 2019 wanafunzi wa elimu ya awali walioandikishwa ni 1,278.816 sawa na asilimia 92.48 ya lengo la kuandikisha wanafunzi 1,382,761.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kati ya hao walioandikishwa wanafunzi 1372 ni wenye mahitaji maaulum. Vilevile wanafunzi wapya walioandikishwa kuanza darasa la kwanza ni 1,670,919. Kati ya hao wanafunzi wenye mahitahi maalum walioandiishwa ni 3028, hatua nzuri na ya kupongezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, naipongeza Wizara pamoja na ofisi ya Rais- TAMISEMI kwa kuendelea kushirikiana na wananchi na wadau wa maendeleo katika kuboresha miundombinu ya shule za awali na msingi. Takwimu zinaonyesha hadi februari 2019 ujenzi wa vyumba vya madarasa 2840 kwa shule za msingi umefanyika na kuongeza idadi ya vyumba vya madarasa 2637 viko katika hatua mbalimbali ya ukamilishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti vilevile jumla ya matundu ya vyoo 7067 vyoo vya wanafunzi matundu 6445 na vyoo vya walimu matundu 622 yamejengwa katika shule za msingi na kuongeza matundu ya vyoo kutoka 190,674 yaliyokuwepo Machi, 2018 hadi kufikia matundu ya vyoo 197,741 mwezi Februari 2019 hili ni ongezeko la asilimia 3.5. Aidha, matundu ya vyoo kutoka 3004 yanaendelea kujengwa na yanatarajiwa kukamilika kabla ya Juni, 2019 ni mwanzo mzuri ambao mwelekeo wake ni kuhakikisha changamotoo zilizokuwepo zinakwenda kuisha kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo Serikali imeendelea kufanya kazi nyingine za uboreshaji miundombinu ya elimu zilizofanyika ni pamoja na ujenzi wa nyumba za walimu 720 na kuongeza idadi ya nyumba hizo kutoka 44320 mwaka 2018 hadi nyumba 45040 Februari, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, jambo lingine la kupongeza ni idadi ya madawati ya wanafunzi watatu watatu kuongeza kutoka madawati 2,858,982 yaliyokuwepo Machi,2018 hadi madawati 2,994,266 Februari 2019 sawa na ongezeko la madawati 135,284. Aidha, kupitia programu ya Equip-T, Serikali imetoa jumla ya vyumba vya madarasa yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi yametekelezwa katika mikoa tisa yenye halmashauri 63. Yapo mengi sana yaliyofanywa na yanayoendelea kutekelezwa na Serikali yangu sikivu ya Chama cha Mapinduzi katika sekta hii ya elimu, naishauri Serikali kuendelea kuboresha maeneo mbalimbali kwenye sekta ya elimu, hii ni kutokana na umuhimu wake hasa katika maendeleo endelevu ya kiuchumi na mapinduzi ya nchi ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kugusia sasa changamoto zinazohusu sekta ya elimu katika Jimbo la Kibaha Vijijini, ni mdau mkubwa wa sekta hii ya elimu, nimekuwa nikihamasisha wananchi wangu kuhakikisha wanachangia sekta ya elimu, halikadhalika na mwenyewe nikishiriki kama mfano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imejitahidi kufanya mengi sana kwenye sekta hii na mengi hayo ni mazuri yenye tija, lakini bado Kibaha Vijijini tuna changamoto mbalimbali katika sekta ya elimu, tuna changamto ya upungufu wa nyumba za walimu 342, upungufu wa vyumba vya madarasa 140, matundu ya vyoo 483 nadawati, ofisi za walimu 27 pamoja na samani za ofisi, naiomba Serikali katika bajeti hii kuliangalia hili na kuongeza fedha kwenye bajeti hii hasa katika halmashauri yangu ili kutatua changamoto katika jimbo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, fedha husika zifike kwa wakati ili ziende moja kwa moja katika changamoto husika na kuzitatua. Aidha, tuna changamoto ya mabweni ya shule ya Magindu na bwalo la Shule ya Sekondari ya Soga na kupanda madaraja kwa walimu wetu, pamoja na walimu kupanda madaraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika bado pia kuna changamoto kubwa jimboni kwangu ya ucheleweshaji wa fedha za uhamisho wa walimu wetu pindi wanapopata uhamisho, hali hiyo imekuwa ikirudisha nyuma hamasa kwa walimu kwani fedha hizo za uhamisho zinapochelewa husababisha walimu kutokufika katika vituo vyao vya kazi kwa wakati,naiomba wizara kuifanyia kazi changamoto hii, na kwenye majumuisho ya majibu wakati wizara itakapotoa majumuisho naomba kupata majibu ya changamoto hii, ni lini walimu wangu wanaodai fedha za uhamisho watapatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuwepo mahali hapa nami niweze kuchangia hotuba hii ya Bajeti ya Wizara ya Kilimo ya Mwaka 2019/2020. Vilevile nichukue fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri na watendaji wake wa Wizara kwa kuandaa hotuba nzuri, hotuba hii inakwenda kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi kwa kuhakikisha sekta nzima ya kilimo inaendelea kuimarika kama ilivyoainishwa hasa ukizingatia nchi yetu ina uzalishaji mkubwa wa mazao ya chakula.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kuanza kwa kutoa pongezi zangu kubwa kwa Serikali, hakika Serikali imeendelea kuweka jitihada za kutosha katika sekta nzima ya kilimo. Hali ya uzalishaji wa mazao ya chakula kwa msimu wa 2017/2018 na upatikanaji wa chakula kwa mwaka 2018/ 2019 imeendelea kuimarika kutokana na hali nzuri ya mvua katika maeneo mengi ya nchi, kuongezeka kwa tija na uzalishaji. Uzalishaji wa mazao ya chakula umefikia tani milioni 16.89 ikilinganishwa na mahitaji ya chakula ya tani milioni 13.57. Hivyo nchi ina ziada ya chakula ya tani milioni 3.32 za mazao yote. Hii ni hatua nzuri na ya kujivunia kwa usalama wa chakula ni usalama wa nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi nyingine kwa Serikali ni Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II). Tarehe 4 Juni, 2018 Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alizindua Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II). Programu hiyo inalenga kuleta mageuzi katika sekta ya kilimo; kwa maana ya mazao, mifugo na uvuvi; ili kuongeza uzalishaji na tija, kufanya kilimo kiwe cha kibiashara na kuongeza pato la wakulima, hususan wakulima wadogo kwa ajili ya kuboresha maisha na usalama wa chakula na lishe, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ASDP II.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali imeimarisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) ili kuwa benki mama itakayoongoza mipango inayolenga kutatua changamoto ya ukosefu wa mitaji kwa wakulima, wafugaji na wavuvi nchini. Lengo la Serikali ya Chama Cha Mapinduzi ni kuifanya TADB kuwa benki ya mfano na ya kisasa katika kuleta mapinduzi ya kilimo nchini kutoka katika kilimo cha mazoea cha kujikimu kwenda katika kilimo cha kibiashara na uzalishaji wenye tija katika kukuza uchumi na kupunguza umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo la kujivunia sana, hadi kufikia Februari, 2019 TADB imetoa mikopo ya shilingi bilioni 100.7 ikilinganishwa na shilingi bilioni 10 mwaka 2017. Mikopo hiyo imewanufaisha zaidi ya wakulima na wafugaji milioni moja nchi nzima. Aidha, TADB tayari imeshafungua ofisi mbili za kanda Jijini Dodoma na Mwanza.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa menejimenti na Bodi ya TADB ni kukamilisha ufunguzi wa ofisi zilizopangwa kwa wakati ili kutatua changamoto za upatikanaji wa pembejeo na miundombinu duni ya uzalishaji, usafirishaji, uchakataji wa mazao na masoko zinazokabili wakulima wadogo nchini; kama Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyotangulia kuzungumza katika hotuba yake.

Mheshimiwa Spika, uzalishaji wa mazao makuu ya biashara ya kimkakati yakiwemo chai, kahawa, korosho, pamba na tumbaku umeimarika kutokana na juhudi zinazofanywa na Serikali ikiwemo kuimarisha ushirika. Kwa mfano, uzalishaji wa zao la pamba uliongezeka kutoka tani 132,934 mwaka 2017/2018 hadi kufikia tani 222,039 mwaka 2018/2019, wakati uzalishaji wa zao la kahawa uliongezeka kutoka tani 45,245 hadi kufikia tani 65,000.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutoa kipaumbele kwa mazao hayo na mengine kwa kuwa ndiyo mhimili wa kutoa malighafi za kuendesha viwanda na yana mnyororo mpana wenye fursa ya kutoa ajira nyingi na kuliingizia taifa fedha za kigeni. Mfano, katika mkakati wa uzalishaji wa zao la chikichi Serikali kwa kweli imekuwa ikitumia fedha nyingi za kigeni kwa ajili ya kununua mafuta ya kula kutoka nje ya nchi. Aidha, uzalishaji mdogo wa zao la chikichi ni miongoni mwa sababu za kushindwa kujitosheleza kwa mahitaji ya mafuta ya kula nchini. Kutokana na changamoto hiyo Serikali imeamua kuweka nguvu kubwa kwenye uzalishaji wa mazao ya mbegu za mafuta ili kuondokana na utegemezi na kuokoa matumizi ya fedha za kigeni.

Mheshimiwa Spika, sina budi kuendelea kuishukuru Serikali kwa kuchukua hatua mbalimbali za kutatua changamoto za wakulima jimboni kwangu. Hata hivyo bado kuna baadhi ya maeneo kumeendelea kuwepo changamoto za migogoro ya wakulima na wafugaji. Migogoro hiyo baadhi yake imekuwa ikilalamikiwa na wakulima kwa baadhi ya maamuzi yanayochukuliwa na kuonekana kesi nyingi zikiwapendelea wafugaji.

Naiomba Wizara kuchukua hatua madhubuti hasa katika kipindi hiki kwa kuangalia namna gani itaweza kutatua migogoro hiyo kwa kuhakiki mipaka ili maeneo ya wakulima na wafugaji yajulikane. Kufanya hivyo kutasaidia kumaliza tatizo kubwa lililopo jimboni kwangu la migogoro hii. Aidha, kuna madai ya muda ya wakulima wa zao la korosho wa Soga, Kikongo na kadhalika. Wakulima hawawana madai yao kwa Serikali, ni fedha za malipo kwa ajili ya zao la korosho. Sasa namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa akihitimisha hotuba yake anipe majibu ya changamoto hizi ili wananchi wangu wapate kujua hatma ya maswali wanayojiuliza.

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika kuna tatizo katika mradi wa Shamba la Umwagiliaji la Mongomole, Kwala. Mradi huu umetumia fedha nyingi na inasemekana kuna ubadhirifu mkubwa umefanyika. Nakuomba Mheshimiwa Waziri atupe majibu juu ya mradi huu na tuhuma hizi. Je, Serikali inatambua hilo na hatua gani za haraka itakwenda kuzichukua, kwani mradi huu umetumia fedha nyingi na umekuwa hauna tija kwa wananchi?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.