Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Tunza Issa Malapo (1 total)

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri Mkuu, TMA imekuwa ikijitahidi sana kutoa taarifa sahihi kuhusu uwepo wa mvua kubwa nchini kwetu na Serikali ina vyombo vyake vingi vya kujua kwamba mvua inanyesha kubwa sehemu gani. Sasa, badala ya kuacha utashi wa mzazi aseme nimpeleke mtoto wangu shule au nisimpeleke, kwa nini zile mamlaka zetu kule chini zisiwe zinatoa taarifa kwamba leo Mtwara kuna mvua kubwa, watoto wote wasiende shuleni ili kuepusha maafa ambayo yanatokea na yanawakumba watoto wetu?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kama nilivyosema kwamba, Serikali yetu imefanya uwekezaji mkubwa sana kwenye mfumo wa utoaji taarifa ya hali ya hewa kila siku hapa nchini. Taarifa hizi ambazo zinatokana na mitambo na wataalam walioko kwenye sekta zinatakiwa zizingatiwe pia na mamlaka zote mpaka kule vijiji. Kwa hiyo ni jukumu la mamlaka zetu ambazo pia ni Kamati za Maafa kutoa taarifa za hali ya hewa ili kuepusha maafa hayo kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa maelekezo hapa kwa halmashauri zote nchini na mikoa kwa kupitia wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya, wahakikishe kuwa wanajenga utamaduni wa kutoa mawasiliano wakati wote pindi wanapopata taarifa za hali ya hewa. Kama taarifa ya hali ya hewa hiyo inaweza kuwa mbaya kwenye eneo hilo, basi ni wajibu wa Mkuu wa Mkoa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, bado narudia tena kuwasihi na kuwataka Wakuu wa Mikoa kufuatilia mwenendo wa hali ya hewa hasa kipindi hiki ambacho kinaonesha kwamba mvua zitaendelea kuwa kubwa mpaka mwezi Mei, waweze kujua, je, kwenye mkoa wao hali ya hewa ikoje na waweze kutumia njia hiyo kuweza kutoa taarifa kwa wananchi wao kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, naendelea kusisitiza viongozi wetu walioko mikoani kuhakikisha kwamba wanatoa taarifa hizi mara kwa mara na ndio wajibu wao ili kuweza kuokoa hali hii ambayo watu wengine walikuwa hawapati taarifa huku mamlaka zetu za Serikali zikiwa ziko pale.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nalichukua hili kwa ajili ya kuendelea kuliimarisha zaidi kwenye kipindi hiki ambacho mvua zinaendelea kuwa nyingi. Ahsante sana. (Makofi)