Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Tunza Issa Malapo (26 total)

MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Sera Mpya ya Elimu ya mwaka 2014 inatambua upatikanaji wa elimu ya msingi bure; lakini Serikali imeshindwa kupeleka ruzuku ya shilingi 10,000 kwa kila mwanafunzi wa shule za msingi za umma na shilingi 25,000/= kwa kila mwanafunzi wa shule za sekondari za umma:-
Je, Serikali inaweza kuweka mchanganuo wa jinsi gani itakavyoweza kutekeleza Sera ya Elimu ya mwaka 2014 kwa kutoa elimu bure bila kuathiri ubora wa elimu?
NAIBU WAZIRI WA TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malopo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli fedha za uendeshaji wa elimu (capitation) zikiwemo shilingi 10,000/= kwa wanafunzi wa shule ya msingi na shilingi 25,000/= kwa wanafunzi wa sekondari zilikuwa hazipelekwi kwa ukamilifu. Kwa sasa Serikali imeamua kuanzia Januri, 2016 wanafunzi wote walioandikishwa darasa la kwanza na wale walioandikishwa kidato cha kwanza pamoja na wale wanaoendelea na shule gharama zilizokuwa zinagharimiwa na wazazi au walezi kwa kulipia ada na michango mbalimbali sasa zitalipwa na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanzia Serikali imetenga shilingi bilioni 131.4 ikiwa ni fedha za ruzuku ya uendeshaji wa shule, chakula, mitihani na fidia ya ada. Fedha hizo zitapelekwa moja kwa moja shuleni kutoka Hazina kwa wastani wa shilingi bilioni 18.77 kila mwezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizo zinahusisha shilingi 10,000/= kwa wanafunzi wa shule ya msingi kwa mwaka, shilingi 25,000/= kwa mwanafunzi wa sekondari kwa mwaka, shilingi 1,500/= kwa kila mwanafunzi kwa shule za msingi na sekondari kwa ajili ya chakula, fidia ya ada ya shilingi 20,000/= kwa wanafunzi wa kutwa na shilingi 70,000/= kwa wanafunzi wa bweni kidato cha kwanza hadi cha nne kwa mwaka. Tayari Serikali imeshapeleka shilingi bilioni 18.77 kwa mwezi Januari, 2016.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Serikali inatambua umuhimu wa barabara; na barabara inayounganisha Mtwara Mjini, Nanyamba, Tandahimba, Newala hadi Masasi haipitiki vizuri wakati wote na hivyo kuwafanya wananchi waone kama wametengwa na Serikali yao.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) ilisaini mkataba na Mkandarasi Mshauri Multi Tech Consult (pty) Ltd. kutoka Botswana akishirikiana na Unitec Civil Consultants Ltd ya hapa nchini tarehe 15 Mei, 2014 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Mtwara Mjini – Nanyamba – Tandahimba – Newala na hadi Masasi yenye urefu wa kilometa 210 kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami kwa gharama ya shilingi milioni 1,280,832. Usanifu wa kina wa barabara hii ulikamilika mwezi Aprili, 2015.
Taratibu za kumpata Mkandarasi wa kujenga kwa kiwango cha lami sehemu ya Mtwara hadi Mnivata ambapo ni kilometa 50, zipo katika hatua za mwisho ambapo ujenzi utaanza mara baada ya mkataba kusainiwa. Aidha, ujenzi wa sehemu iliyobaki kati ya Mnivata na Masasi, utafanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha na kwa kuzingatia kwamba barabara hii imeahidiwa katika ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 hadi 2020 na wakati huo huo iliahidiwa na Mheshimiwa Rais ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Awamu ya Nne na wa Awamu ya Tano. Kwahiyo, tutaijenga.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri, tunaomba utusomee tena hicho kiasi ulichosoma kwenye majibu.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni shilingi 1,280.832 au shilingi bilioni 1.280.832.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Wananchi wa Jimbo la Nanyamba kwa muda mrefu wamekuwa wakipata shida ya ukosefu wa maji safi na salama:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha wananchi hao wanapata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalumu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango wa kufanya upanuzi wa mradi wa maji wa Kitaifa wa Makonde kutokea katika Kijiji cha Chikunda kupitia Kijiji cha Nyundo hadi Dihamba. Wakazi wapatao 49,206 waishio katika Vijiji 49 vya Halmashauri ya Nyanyamba na Vijiji saba vya Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara watanufaika na mradi huo utakapokamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na tathmini ya awali, upanuzi wa mradi huo utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 11.4. Utekelezaji wa mradi huo unategemea upatikanaji wa fedha zitakazotengwa na Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Halmashauri ya Nanyamba ina mpango wa kufanya ukarabati wa miundombinu ya bomba katika miradi ya maji iliyojengwa kwa ufadhili wa AMREF ipatayo 17 inayotumia nishati ya nguvu za jua. Ukarabati huo unatarajiwa kugharimu shilingi milioni 719 na unakadiriwa kuwanufaisha wakazi wapatao 15,433 waishio katika Jimbo la Nanyamba na hivyo kuongeza kiwango cha upatikanaji wa huduma ya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Halmashauri ya Mtwara Vijijini inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji ya Mbembelo - Mwang‟anga na Nanyamba - Maranje. Miradi hii itanufaisha Vijiji vya Mwang‟anga, Mbembaleo, Mwamko, Maranje, Mtimbwilimbwi, Mtopwa, Mtiniko, Shaba, Mbambakofi na Mnivata vyenye wakazi wapatao 20,166. Miradi hii itakapokamilika upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa Halmashauri ya Nanyamba utaongezeka kutoka asilimia 43 hadi asilimia 80.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA (K.n.y MHE. TUNZA I. MALAPO) aliuliza:-
Dhana ya elimu ni majumuisho ya mambo mengi sana ikiwemo matibabu ya huduma ya kwanza, gharama za umeme, maji, vyakula (kwa shule za bweni), posho za walimu (part time) pamoja na zana za kufundishia zisizohifadhika kwa muda mrefu; na nyingi kati ya gharama hizo zilikuwa zinatatuliwa mashuleni na Wakuu wa Shule kwa kutumia ada na michango waliyokuwa wanatoza wanafunzi.
Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha ufanikishwaji wa dhana hii ya elimu bure bila kuanzisha migogoro mipya kati ya wakuu wa shule, walimu, wazazi pamoja na wanafunzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, dhana ya utoaji wa elimu bila malipo inatokana na Sera ya Elimu na mafunzo ya mwaka 2014 inayoelekeza utaratibu wa ugharamiaji wa elimu ya awali kuwa ya lazima kuanzia shule za msingi hadi sekondari kidato cha nne.
Mheshimiwa Naibu Spika, elimu msingi bila malipo inazingatia uendeshaji wa shule bila ada wala michango ya aina yoyote ya lazima kutoka kwa wazazi au walezi wa wanafunzi. Hata hivyo, elimu bila malipo haiondoi dhamira ya uzalendo kwa jamii ya kushiriki kwa hiari kuchangia kwa hali na mali katika kuleta maendeleo ya elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kupeleka shilingi bilioni 18.777 kila mwezi kwa ajili ya kugharamia mpango huu. Fedha hizo zinatumika kugharamia mitihani ya Taifa, chakula cha wanafunzi wa bweni, ada ya mwanafunzi kwa shule za kutwa na bweni na fedha za uendeshaji wa shule za msingi na sekondari.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejipanga ili kuhakikisha kuwa utoaji wa elimu bila malipo ambao umeshaanza kwa shule zote za umma nchini hausababishi migogoro kati ya wakuu wa shule, walimu, wazazi pamoja na wanafunzi. Ili kuhakikisha hilo halitokei Serikali imetoa miongozo mbalimbali katika mikoa yote inayofafanua kuhusu utekelezaji wa mpango huo.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Je, gharama ya ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam ni shilingi ngapi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara na Songo Songo Mkoani Lindi hadi Dar es Salaam ulianza kutekelezwa mwezi Juni, 2013 na kukamilika mwezi Oktoba, 2015. Ujenzi wa mradi huu ulihusisha ujenzi wa mitambo ya kuchakata gesi asilia yaani Madimba (Mtwara) pamoja na Songo Songo (Lindi) kwa gharama ya dola za Marekani milioni 349.51 na pia ujenzi wa bomba la kusafirishia gesi asilia kutoka Mtwara na Songo Songo – Lindi hadi Dar es Salaam kwa gharama ya dola za Marekani milioni 875.72.
Mheshimiwa Spika, jumla ya gharama zote za mradi huu hadi kukamilika ni dola za Marekani milioni 1,225.23.
Mheshimiwa Spika, bomba lina uwezo wa kusafirisha gesi asilia futi za ujazo milioni 784 kwa siku na linaweza kufikia futi za ujazo milioni 1,002 kwa siku. Kwa sasa gesi inayosafirishwa ni futi za ujazo milioni 68.5 kwa siku.
MHE. HAWA B. MWAIFUNGA (k.n.y. MHE. TUNZA I. MALAPO) aliuliza:-
Je, ni eneo gani limetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Kiwanda cha Kubangua Korosho katika Manispaa ya Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani imetenga maeneo kwa ajili ya viwanda vya kubangua korosho kwa ajii ya wajasiliamali wadogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2014/2015 mpaka mwaka 2016/2017 Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani ilipanga na kupima viwanja vyenye ukubwa wa ekari 239.13 katika eneo la Mtepwezi na Mtawanya kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya kubangua korosho na maghala. Katika viwanja hivi jumla ya ekari 28.41 imegawiwa kwa mfumo wa wakfu wa kuhudumia zao la korosho (CIDTF) na Chama cha Ushirika cha Mtwara na Masasi (MAMCU) kwa ujenzi wa viwanda vya korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ina jumla ya ekari 210.72 ambazo zipo tayari kwa ajili ya waombaji mbalimbali walio tayari kujenga viwanda hasa vya kuchakata korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Halmashauri inaendelea na utengaji wa maeneo kwa ajili ya ujasiliamali wadogo wadogo kwa mwaka 2016/2017. Halmashauri imetenga eneo lenye ukubwa wa ekari 7.8 kwa ajili ya wajasiliamali. Maeneo hayo yapo eneo la Chikongola, Skoya, Ufukoni A, Ufukoni Stendi na eneo la SIDO.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Je, ni lini tatizo la kukatika mara kwa mara kwa umeme katika Mkoa wa Mtwara litaisha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara katika Mikoa ya Mtwara na Lindi inayopata umeme katika kituo cha kuzalisha umeme kutumia gesi asilia kilichopo Mkoani Mtwara kulitokana na kuharibika kwa mitambo ya kuzalishai umeme iliyochangiwa na uchakavu wa mitambo hiyo pamoja na urefu wa miundombinu ya kusambaza umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) imechukua hatua mbalimbali ili kutatua tatizo la kukatika kwa umeme katika mikoa hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua hizo ni pamoja na kutekeleza mradi wa ujenzi wa vituo viwili vya kukuza na kupoza umeme vyenye uwezo wa 132/33KV na 20MVA vilivyopo Mtwara Mjini na Mahumbika Mkoani Lindi, pamoja na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolt 132 ya umbali wa kilomita 80 kutoka Mtwara hadi Mahumbika. Mradi huu umekamilika na umeanza kufanya kazi rasmi mwezi Mei, 2018 na gharama ya mradi ni shilingi bilioni 16.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO imekamilisha ukarabati wa mitambo minane na mtambo mmoja uliosalia, Mzabuni wa Kampuni ya MANTRAC anaendelea na kazi ya kukarabati na inatarajia kukamilika mwezi Juni, 2018. Ili kukabiliana na ongezeko la mahitaji ya umeme katika Mikoa ya Mtwara na Lindi, TANESCO imenunua generator mbili zenye uwezo wa kufua umeme wa megawatts 4 na kazi ya kufunga mitambo hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua nyingine Mikoa ya Lindi na Mtwara imeunganishwa na Gridi ya Taifa kupitia njia ya umeme ya kilovolti 33 ambapo Mikoa hiyo sasa inapata umeme kutoka kituo cha kuppoza umeme cha Mbagala na hatua hii imeimarisha hali ya upatikanaji wa umeme na hivyo kukipunguzia mzigo kituo cha kuzalisha umeme cha Mtwara.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Mji Mkongwe wa Mikindani uliopo katika Manispaa ya Mtwara Mikindani unakuwa kivutio cha utalii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wizara imeweka mkakati mahsusi wa kuendeleza Mji Mkongwe wa Mikindani na kuutangaza ndani na nje ya nchi kama kivutio cha utalii. Mwaka 2016 Wizara kupitia Idara ya Mambo ya Kale ilianzisha kituo kipya cha mambo ya kale ndani ya Mji wa Mikindani. Kwa kuanzia Wizara imepeleka watumishi wawili na itaendelea kuongeza idadi ya watumishi kadri upatikanaji utakavyokuwa. Kituo hicho kimelenga kusimamia uhifadhi na matumizi endelevu ya malikale zinazopatikana katika Mji Mkongwe wa Mikindani. Aidha, mwaka 2017 kupitia Tangazo la Serikali namba 308 Wizara ilitangaza mji huu kuwa urithi wa utamaduni wa Taifa. Mji Mkongwe wa Mikindani ni kati ya maeneo…
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka Madaktari wa kutibu magonjwa mbalimbali katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara ya Ligula?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeajiri Madaktari 11 katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara katika ajira mpya za mwezi Julai, 2018. Kwa sasa hospitali imeshapokea Madaktari nane na kufanya jumla ya Madaktari wa kada kuwa 17. Sanjari na hilo, katika kupunguza tatizo la uhaba wa Madaktari Bingwa, Hospitali ya Ligula kwa kupitia utaratibu wa kuendeleza watumishi wake inatarajia kumpokea Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Koo, Pua na Maskio (ENT Surgeon) ambaye anatarajiwa kumaliza mwezi Oktoba, 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, katika kipindi cha Mwaka wa Fedha 2017/2018, Wizara iliwapeleka Madaktari Bingwa wa fani ya Upasuaji wa Kawaida na Mifupa (General Surgeon na Orthopaedic Surgeon) katika Chuo cha Muhimbili ambapo wanatarajia kumaliza katika kipindi cha mwaka wa fedha 2020/2021. Aidha, Wizara itaendelea kutenga bajeti ya kuwasomesha Madaktari Bingwa wa fani mbalimbali ili kufikia azma ya Serikali na kuhakikisha kwamba hospitali zote za rufaa za mikoa zinakuwa na Madaktari Bingwa wa kutosha.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, Serikali inatumia Sheria ipi kutowapa wafanyakazi stahiki zao zinazohusu kupandishwa madaraja na ongezeko la mwaka (Annual Increment) kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Barua ya Katibu Mkuu – Utumishi yenye Kumbukumbu Namba CAC. 45/257/01/E/83 ya tarehe 9 Septemba, 2013 kuhusu upandishwaji wa vyeo kwa madaraja kwa watumishi wote nchini wa umma huzingatia vigezo muhimu sana kama vile sifa za kitaaluma, uzoefu wa kazi, utendaji mzuri wa kazi kwa maana ya OPRAS, tange au ukubwa kazini kwa maana ya Seniority, uwepo wa ikama na bajeti iliyoidhinishwa kwa mwaka husika wa fedha, vilevile bila kusahau nidhamu na mwenendo wa mtumishi huyo wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kanuni ile ya E. 9(1) ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009, Toleo la Tatu, nyongeza ya mwaka ya mishahara haipaswi kuombwa au kudaiwa na watumishi wa umma bali Serikali ndio yenye uamuzi wa kutoa au kutokutoa nyongeza hiyo. Hivyo, katika utumishi wa umma hakuna sheria inayoainisha kwamba, mtumishi anatakiwa kupata nyongeza ya kawaida ya mshahara kwa kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kanuni ya E.2 ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009 viwango vya mshahara ikiwa ni pamoja na nyongeza ya mshahara kwa kila mwaka kwa maana ya annual increment hupangwa kulingana na uwezo wa Serikali kulipa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilitoa nyongeza ya mshahara ya kila mwaka kwa maana ya annual increment kwa watumishi wote wa umma kuanzia mwezi Novemba, 2017. Vilevile Serikali imewaelekeza waajiri wote kuendelea na upandishwaji vyeo kwa watumishi 193,166 waliokasimiwa katika ikama ya bajeti ya mwaka 2017/208 kuanzia tarehe 1 Mei, 2019 na barua zinaendelea kuingizwa kwenye mfumo wa taarifa za kiutumishi na mishahara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahimize watumishi wote wa umma kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kuleta tija katika utumishi wa umma na Serikali itaendelea kutoa nyongeza ya mshahara pamoja na kuboresha mazingira ya kazi kadri uwezo wa Serikali kulipa utakavyoruhusu. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka x-ray machine mpya katika Hospitali ya Rufaa ya Mtwara – Ligula?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mtwara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Hospitali ya Ligula inakabiliwa na uchakavu wa mashine ya x- ray ambayo uharibika mara kwa mara. Katika ziara yangu ambayo niliifanya katika hospitali hii mnamo tarehe 4 Disemba, 2018 nilijionea uchakavu wa mashine na hivyo tulitoa ahadi ya Serikali ya kuipatia hospitali hii mashine mpya ya digital x-ray.

Mheshimiwa Spika, mashine tano mpya za x-ray za kidijitali (digital x-ray) zimeshaingia nchini kupitia utaratibu wa managing equipment services tarehe 14 Januari, 2020. Taratibu za ugomboaji zikikamilika zitapelekwa na kusimikwa katika Hospitali za Rufaa za Njombe, Iringa, Tabora, Temeke pamoja na Mkoa huu wa Mtwara katika Hospitali ya Ligula.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, ni Watumishi wangapi wanahitajika na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili Mamlaka hiyo iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo Mbunge Viti maalum kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili Mamlaka ya Mapato Tanzania iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi inahitaji watumishi wapatao 7,000 wa kada mbalimbali za kiutumishi.
MHE. TUNZA I. MALAPO Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafufua viwanda vyote vya kubangua Korosho vilivyopo Manispaa ya Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kabla ya zoezi la Ubinafsishaji, Serikali ilikuwa na jumla ya viwanda 12 vya kubangua korosho nchini. Kati ya viwanda hivyo viwanda viwili vilikuwa katika Manispaa ya Mtwara. Hiki ni kile kilichokuwa kinajulikana kama Likombe Cashew Factory na hivi sasa ni Micronics Systems Company Limited; na kile kilichokuwa kinaitwa Mtwara Cashew Company Limited, sasa hivi ni Cashew Company (2005) Limited.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda hivi vyote viwili vinafanya kazi. Kiwanda cha Micronics Systems Company Limited kina uwezo uliosimikwa wa kubangua korosho tani 5,000 kwa mwaka. Hata, hivyo kutokana na changamoto ya malighafi kiwanda hicho kinabangua wastani wa tani 2,000 kwa mwaka. Pia Kiwanda cha Mtwara Cashew Company Limited kinaendelea na uzalishaji katika kutoa huduma za kupanga madaraja (grading) na kufungasha (packaging) kwa korosho zinazobanguliwa na viwanda vidogo vilivyopo katika maeneo hayo ambavyo havina mitambo ya grading na packaging.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi ili kuvutia uwekezaji na kuwezesha sekta binafsi kuwekeza katika viwanda vipya na kufufua viwanda vilivyopo vya kubangua korosho hapa nchini.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya kujaa maji mara tu mvua zinaponyesha katika baadhi ya maeneo ya Kata za Magomeni, Shangani, Ufukoni, Reli na Likombe katika Manispaa ya Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya kujaa maji mvua zinaponyesha katika baadhi ya maeneo ya Kata za Magomeni, Shangani, Ufukoni, Reli na Likombe katika Manispaa ya Mtwara Mikindani. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali kupitia Mradi wa Uendelezaji Miji (Tanzania Strategic Cities Projects) imejenga mifereji ya kutoa maji kwa maana ya stand-alone drains yenye urefu wa kilomita 10 kwa gharama ya shilingi bilioni 1.82 katika Kata za Shangani, Reli, Likombe na Vigaeni Manispaa ya Mtwara Mikindani.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kukamilisha Mpango Kabambe wa kuyaondoa maji ya mvua katika makazi na kuyaelekeza baharini katika Manispaa ya Mtwara Mikindani. Serikali itatafuta fedha ili kutekeleza kikamilifu Mpango Kabambe wa kuondoa maji ya mvua kwenye makazi na kuyaelekeza baharini katika Manispaa ya Mtwara Mikindani.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaunganisha mfumo wa gesi asilia kwa ajili ya kupata nishati ya kukaangia samaki katika Soko la Feri Manispaa ya Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) inaendelea na kazi ya ujenzi wa miundombinu ya kusambaza gesi asilia katika mikoa mbalimbali nchini ukiwemo Mkoa wa Mtwara kwa ajili ya matumizi ya viwandani, majumbani na taasisi za umma na binafsi. Katika Mkoa wa Mtwara, mradi huu unahusisha ujenzi wa miundombinu ya kusambaza gesi asilia kwa njia za mabomba na vituo vya kuongeza mgandamizo wa gesi (Compressed Natural Gas (CNG) Stations).

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia katika Soko la Feri katika Manispaa ya Mtwara Mikindani upo katika hatua ya kukamilisha usanifu wa kina wa kihandisi, utakaofuatiwa na hatua ya kumpata mkandarasi wa ujenzi wa mradi huo. Kazi ya usanifu inatarajiwa kukamilika mwezi Agosti, 2021 na ujenzi kuanza Desemba, 2021 na kukamilika Juni, 2022. Gharama za mradi ni takribani shilingi bilioni 10.11.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Bandari ya Uvuvi na kununua Meli ya uvuvi katika Mkoa wa Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo Mbunge wa Mtwara Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa Ujenzi wa Bandari ya Uvuvi ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uvuvi ya Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 – 2025 Ibara 43(a) ambazo zimeainisha kujenga Bandari ya Uvuvi katika Ukanda wa Pwani ambayo itawezesha meli zinazovua Bahari Kuu kutia nanga kwa lengo la kushusha samaki na mazao ya uvuvi, kuuza samaki, kutoa takwimu sahihi na huduma nyinginezo ikiwemo kujaza mafuta, vyakula na matengenezo madogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutekeleza Mpango huo, Serikali iliingia mkataba na mshauri elekezi ili kubaini eneo linalofaa kwa ujenzi wa bandari. Baada ya uchambuzi huo, mshauri elekezi alipendekeza bandari ijengwe katika eneo la Mbegani – Bagamoyo, na kazi hiyo itaanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na mahitaji na uwepo wa bajeti Serikali itaendelea kutazama uwezekano wa kujenga Bandari za Uvuvi katika maeneo mengine ikiwemo Mkoa wa Mtwara kwa siku za usoni ikiwa ni pamoja na kuboresha mialo, kuimarisha vikundi wa usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi na kuanzisha Vyama Vya Ushirika wa Wavuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwekezaji na ujenzi wa Bandari za Uvuvi utawezesha kukua kwa biashara na shughuli za uvuvi Ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi ikiwemo Mkoa wa Mtwara.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni lini Hospitali ya Kanda ya Kusini itaanza kutoa Huduma kwa Wananchi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu: -

Mheshimiwa Spika ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Mlapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Kanda ya Kusini Mtwara imewekewa jiwe la msingi tarehe 26/07/2021 na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango na huduma zimeanza tarehe 1 Oktoba, 2021. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kufanya utafiti kuhusu hali ya biashara na uchumi wa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka utaratibu wa kupata matokeo ya tafiti zinazolenga kuboresha biashara na uchumi wa wananchi pamoja na kuwaunganisha wananchi na fursa za masoko kupitia maonesho ya mifuko na programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, aidha, pamoja na hiyo mikakati mingine ni kutoa tuzo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya tafiti bora kwenye masuala ya uchumi na biashara.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kufufua kilimo cha zao la muhogo katika Mkoa wa Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ilianzisha Mradi wa Kufufua Zao la Muhogo katika Kanda ya Ziwa Victoria na Kanda ya Pwani ukiwemo Mkoa wa Mtwara mwaka 2015. Awamu ya Kwanza ya mradi huo iliisha mwanzoni mwa mwaka 2021, awamu ya pili imeanza Disemba, 2021 na inategemewa kwisha mwaka 2024. Kupitia mradi huu uzalishaji wa muhogo katika Mkoa wa Mtwara umeongezeka kutoka tani 611,210 kwa mwaka 2016/2017 hadi tani 866,676 kwa mwaka 2019/2020.

Mheshimiaw Spika, kutokana na kuongeza utoaji wa huduma za ugani na uzalishaji wa mbegu za muhogo. Jumla ya vipando bora vya muhogo pingili milioni 30.4 kwa mwaka 2019/2020 hadi pingili milioni 40 kwa mwaka 2020/2021 zenye uwezo wa kutoa mavuno mengi kuhimili mabadiliko ya tabia nchi na magonjwa zilizalishwa na kusambazwa kwa wakulima.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni lini chujio la maji linalojengwa katika Manispaa ya Mtwara Mikindani litakamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekamilika ujenzi wa chujio la kuchujia maji mwezi Aprili, 2022. Kukamilika kwa ujenzi wa chujio hilo kumeweza kuboresha upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi katika Manispaa ya Mtwara Mikindani.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukuza utalii wa fukwe za bahari nchini?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII, alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kubuni mikakati mbalimbali ya kuendeleza Mazao mbalimbali ya Utalii, ikiwemo Utalii wa FUKWE. Katika kutekeleza mikakati hiyo, Idadi ya Watalii wanaotembelea fukwe zetu zilizopo katika mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Pwani, Lindi na Mtwara imeendelea kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sambamba na hilo, Serikali imetekeleza yafuatayo: -

i. Kwanza ni kubaini maeneo mapya ya fukwe za Bahari ya Hindi yanayofaa kwa ajili ya uwekezaji wa shughuli za utalii katika Mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Pwani, Lindi na Mtwara;

ii. Lakini pia kuweka utaratibu wa kusajili maeneo ya fukwe yanayofaa kwa shughuli za Utalii kama Maeneo Maalum ya Uwekezaji wa Shughuli za Utalii (Tourism Special Economic Zone); na

iii. Lakini la mwisho ni kuendelea kuwahamasisha wamiliki wa maeneo ya fukwe nchini ili kusajili maeneo ya fukwe wanayoyamiliki chini ya utaratibu wa Maeneo Maalum ya Uwekezaji wa Shughuli za Utalii kwa lengo la kuiwezesha Serikali kushirikiana na wamiliki hao kuhimiza uwekezaji wa utalii wa fukwe.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni kwa kiasi gani Mkoa wa Mtwara umewekeza na unanufaika na uchumi wa Bluu?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ili kuufanya Mkoa wa Mtwara kunufaika na uchumi wa bluu, Serikali imeimarisha miundombinu ya Bandari ya Mtwara na kuifanya kuwa ndiyo kituo kikuu cha usafirishaji wa bidhaa na malighafi mbalimbali. Serikali pia imejenga Kituo cha uzalishaji wa mbegu za mazao ya baharini (majongoo bahari, pweza, kamba na kadhalika) ili kuwasaidia wananchi wa mkoa huo.

Mheshimiwa Spika, vilevile Mamlaka ya Ufundi Stadi (VETA) inatoa mafunzo ya ufugaji wa majongoo bahari na kujenga vizimba vya ufugaji. Aidha, Serikali ya Mkoa wa Mtwara imeelekeza nguvu zake kwenye kilimo cha Mwani katika eneo la Naumo Wilayani Mtwara bila kusahau kilimo cha chumvi ya Bahari.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kuvutia wawekezaji katika uchumi wa Bluu nchini hasa katika sekta za usafirishaji baharini, kilimo, uvuvi, na utalii kwa ajili ya mikoa ya pwani ukiwemo Mkoa wa Mtwara.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, Utekelezaji wa mradi wa Mtwara Corridor umefikia hatua gani?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Ushoroba wa Mtwara (Mtwara Corridor) unajumuisha miradi ya Sekta mbalimbali ikiwa pamoja na Madini, Uchukuzi na Kilimo. Kwa upande wa Sekta ya Uchukuzi, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imetekeleza miradi ya ujenzi wa gati kubwa na la kisasa katika Bandari ya Mtwara lenye urefu wa mita 300. Ujenzi wa Bandari ya Ndubi ambao ulikamilika tangu Desemba, 2021 na Ujenzi wa bandari mpya ya Mbamba Bay ambao upo katika hatua za manunuzi ya Mkandarasi.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali kupitia Shirika la Reli (TRC) imekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa awali kwa ajili ya ujenzi wa reli ya Standard Gauge ya Mtwara - Mbamba Bay na matawi yake kuelekea Liganga na Mchuchuma. Mradi huu unatarajiwa kutekelezwa kwa utaratibu wa ubia kati ya sekta ya Umma na sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na taarifa hizo za miradi, naomba kulifahamisha Bunge lako kuwa, gati jipya lililojengwa katika Bandari ya Mtwara limeanza kuhudumia meli za makasha pamoja na shehena ya Kichele na takriban kila baada ya wiki moja kuanzia tarehe 20/04/2023 limekuwa likihudumia mizigo ya makasha ya yanayokwenda visiwa vya Comoro.

Mheshimiwa Spika, vikao vya wadau wa Ushoroba wa Mtwara vimeanza kuratibiwa chini ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ili kuweka mikakati ya kuendelea kuutangaza zaidi ushoroba huo na kuwavutia wananchi waishio ukanda huo pamoja na nchi jirani kutumia Bandari ya Mtwara na kuufanya ushoroba huo kutumika ipasavyo, ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kufanya utafiti ili kubaini mazao yanayoweza kulimwa na kustawi Mkoa wa Mtwara kama mbadala wa zao la korosho?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Kilimo imeendelea kufanya utafiti katika maeneo ya Mtwara ili kupata mazao mengine zaidi ya korosho ambayo mkulima ataweza kuzalisha ili kuondokana na utegemezi wa zao la korosho pekee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Kilimo kupitia TARI imeendelea kuhamasisha kilimo cha mazao ya muhogo, ufuta, karanga, alizeti, njugumawe, choroko, mbaazi, mtama na kunde ambayo tayari yamefanyiwa utafiti na kuonekana yanafaa kulimwa katika Wilaya zote za Mkoa wa Mtwara. Aidha, Wizara imetoa elimu ya kilimo bora cha mazao hayo ikiwemo matumizi ya mbegu bora, udhibiti wa visumbufu (wadudu waharibifu na magonjwa), kupanda kwa wakati na matumizi sahihi ya mbolea kupitia mashamba ya mfano, radio za kijamii na televisheni.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, ni wanafunzi wangapi wamerejea shuleni tangu waraka wa kuwaruhusu utolewe?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpaka kufikia mwezi Januari, 2023 wanafunzi waliorejea shuleni kuendelea na masomo ya elimu ya sekondari ni 1,907 ambapo waliorudi katika mfumo rasmi ni 562 na waliorejea nje ya mfumo rasmi wa elimu kupitia Mradi wa Kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP) ni 1,345.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa wanafunzi wa elimu ya msingi; Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais - TAMISEMI inaendelea kukusanya taarifa za wanafunzi waliorejea shuleni baada ya kukatiza masomo kwa sababu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakarabati Jengo la OPD na kujenga uzio katika Kituo cha Afya Likombe - Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Likombe ni moja ya vituo vya afya vilivyonufaika na mpango wa maboresho ambapo katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, kituo hicho kilipokea shilingi milioni 500 na kujenga jengo la wazazi, maabara, jengo la kuhifadhia maiti, stoo ya dawa, nyumba ya mtumishi na kichomea taka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maboresho makubwa yaliyofanywa katika kituo hicho, bado kuna uhitaji wa jengo la kuhudumia wagonjwa wa nje (OPD) pamoja na uzio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2024/2025, Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara itatenga shilingi milioni 70 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje katika Kituo cha Afya cha Likombe. Ahsante. (Makofi)