Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Lucy Fidelis Owenya (45 total)

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Serikali imekuwa ikija na Mipango mipya tofauti kila miaka mitano. Je, ni kwa kiasi gani kwa kipindi kilichopita Serikali iliweza kutekeleza Mipango yake? Je, katika Mpango huu vyanzo vya mapato vitapatikana wapi ukizingatia baadhi ya wahisani wamejitoa kusaidia nchi yetu?
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bunge lako Tukufu kila mwaka Serikali imekuwa ikitueleza inataka kuongeza watalii wafike zaidi ya milioni moja wanaoitembelea Tanzania. Nchi yetu ina vivutio vingi sana kupita nchi nyingine Afrika Mashariki, lakini kuja Tanzania ni gharama sana kuliko Kenya, Uganda au Rwanda. Hii inatokana na kutokuwa na usafiri wetu wa anga kutoka nchi za Ulaya na Marekani. Je, Serikali ina mikakati gani ya kufufua Shirika letu la ATCL ili kuweza kuimarisha na kukuza utalii kwa lengo la kupata watalii wengi kuja moja kwa moja mpaka Tanzania badala ya kupitia Kenya inayofanya Utalii wa Tanzania uwe ghali sana?
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa jinsi gani Mpango huu utatekelezwa, kutengeneza reli zetu angalau ziweze kuwa na mabehewa ya mizigo badala ya mizigo na makontena yanayosafirishwa kwenda nchi jirani kama Kongo, Zambia, Rwanda kutumia barabara. Hii inachangia sana kuharibu barabara zetu haziwezi kudumu. Mfano, barabara kutoka Chalinze- Dodoma tu, tayari barabara hii imeharibika kabisa na tangu ijengwe haina hata zaidi ya miaka 20? Serikali itueleze ina mpango gani wa kufufua reli kwa uhalisia siyo kwa maandishi ya hotuba.
Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima, lakini hadi sasa hivi bado kilio chetu ni cha kutegemea mvua na wakulima wengi hawana mitaji. Wengi vijijini bado wanatumia ng‟ombe kulimia na wengi hawapati elimu ya kutosha kuhusu mazao ya biashara na Serikali haisaidii ni kwa jinsi gani itawezesha kuhusu kilimo cha umwagiliaji ili waweze kulima kwa kipindi chote mwaka mzima. Je, Serikali ina mikakati ya kuzalisha mbegu za kisasa hapa nchini ili ziwe kwa bei nafuu?
Mheshimiwa Naibu Spika, mbegu nyingi zinatoka nchi za nje na tukumbuke mbegu kutoka nje zinaagizwa kwa fedha za kigeni ukizingatia fedha yetu thamani yake inashuka kila siku na deni la Taifa linakua kila siku. Je, Serikali inachukua mkakati gani, kuendeleza kilimo ili tuondokane na kilimo cha kutegemea mawingu, kilimo cha jembe la mkono badala ya kuleta kauli mpya kila wakati?
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, michezo ni afya, michezo ni furaha, michezo huondoa mawazo na kadhalika, lakini hapa nchini hakuna viwanja vya michezo. Serikali ya Awamu ya Tano ilisisitiza sana suala la michezo. Je, mmejipangaje kuwapatia wananchi sehemu za kufanyia mazoezi? Kwa mfano katika Manispaa ya Moshi kila mwezi wa tatu tuna mashindano ya kimataifa yajulikanayo kama Kilimanjaro Marathon. Mbio hizi kwa sasa hivi zina washiriki zaidi ya milioni 10 kutoka mataifa mbalimbali lakini tumekuwa tukitumia uwanja wa Chuo cha Ushirika Moshi (MUCOBS) ambacho kwa sasa kinalemewa na wingi wa washiriki wa mbio hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Manispaa ya Moshi tunao uwanja mkubwa wa King George Memorial Stadium ambao kwa sasa unatumika kama soko la kuuzia mitumba. Moshi kuna sehemu nyingi za masoko mfano Pasua, Majengo, Manyema na kadhalika ambako soko hili linaweza kuhamishiwa huko na uwanja wa King George Memorial Stadium ukatumika kwa ajili ya michezo, ukizingatia uwanja ule una michezo tofauti zaidi ya saba. Ni tegemeo langu Serikali itatoa tamko kuhusu kiwanja hiki ili tuweze kudumisha michezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwepo Maafisa Utamaduni lakini bado hawajaweza kutumika ipasavyo katika kukuza utamaduni wetu. Kwa mfano, cultural tourism haijapata msukumo wa kutosha kutoka kwa maafisa hawa. Urithi wetu unaelekea kupotea kwa mfano, ngoma za asili, vyakula vya asili, michezo ya asili, mavazi ya asili hata lugha za asili. Hii ni changamoto kubwa kwa Maafisa Utamaduni hasa ukizingatia tishio la utandawazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kuwa Maafisa Utamaduni wawezeshwe kwa kupewa rasilimali za kutosha ikiwa ni pamoja na vitendea kazi ili waweze kuwafikia walengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, mchakato wa Vazi la Taifa umefikia wapi na mpaka sasa hivi ni kiasi gani cha fedha kilichotumika?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Shirika la Nyumba (NHC), Shirika hili lilianzishwa kwa nia njema ya kusaidia wananchi kujenga nyumba za bei nafuu lakini kwa sasa hivi Shirika hili limekuwa ni la kibiashara zaidi. Hivi huko vijijini hata mijini wananchi wa kipato cha chini wawezaje kumiliki nyumba hata ya milioni 30? Ni vizuri NHC wakijenga nyumba wazipangishe kwa bei nafuu na zile kodi zikishalipwa kwa kipindi cha kutosha kulipia deni la ujenzi ndipo mmiliki apewe offer ya kununua nyumba hiyo kwa bei nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi zinazotozwa na NHC kwa sasa ni za juu sana na baadhi ya nyumba za biashara hazijakarabatiwa lakini kodi zipo juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua ni master plan ipi inayotumika katika Jiji letu la Dar es Salaam? Wananchi wanajenga kama wanavyotaka, lakini ikumbukwe mifumo ya maji taka ni ile ile iliyojengwa enzi ya mkoloni, wakati huo wakazi waliokuwepo walikuwa ni wachache. Sasa hivi Jiji la Dar es Salaam lina wakazi zaidi ya milioni tano wanatumiaje mitandao ile ile ya kupitisha maji machafu? Je, ni kwa kiasi gani Wizara zinashirikiana ili kutatua tatizo hili? Je, Serikali haioni kwa Jiji la Dar es Salaam haiwezi ni wakati muafaka sasa kusitisha ujenzi wa maghorofa makubwa mpaka pawepo na master plan ili mji ujipange? Hakuna hata viwanja vya wazi, viwanja vya michezo nyumba zinasongamana hata emergency ikitokea katikati ya mji siyo rahisi fire brigade kuweza kupita na kuokoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi za majengo. Kodi hizi ni kubwa sana kwa wananchi wa kawaida kuzilipa, nikiungana na Kambi ya Upinzani, kodi hizi zilikuwa zinakusanywa na Halmashauri na hii ilisaidia sana kuweza kuleta maendeleo katika Halmashauri husika. Ni sababu zipi zilipelekea Serikali kuamua kodi hizo zikusanywe na kupeleka Hazina?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kipekee naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na nikiwa kama mdau wa utalii na Mjumbe wa Kamati ya Maliasili na Utalii niweze kuchangia yangu machache. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, utalii unachangia 17.5% kwenye pato la Taifa, lakini tunaweza tukafanya vizuri zaidi kama tutakuwa na mikakati ya kutosha kwanza kwa kuutangaza vya kutosha na pili kuhakikisha kwamba tunagundua utalii mpya. Nimefurahi Mheshimiwa Waziri amesema atatangaza sehemu za utalii Mwanza na kila mahali, lakini naomba nimshauri tu hata hapa Dodoma kuna utalii mzuri tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama naweza nikashauri kuna mawe mpaka Singida. Dodoma tunaweza tukatangaza utalii wa Stone Mountain kama ilivyo Table Mountain South Africa, watu wanaenda kwenye Table Mountain wanatembelea mashamba ya zabibu. Kwa hiyo, wanaweza wakapita hapa kama destination ya a day tour, wakifika hapa watatembelea hiyo Stone Mountain, watatembelea zabibu, wanaweza wakatembelea Chuo Kikuu na attraction ya Bunge as well. Kwa hiyo, watu wa Dodoma nao wanaweza wakapata mapato kutokana na utalii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaweza tukawa na watalii throughout the year kuanzia Januari mpaka Disemba lakini ningemwomba Mheshimiwa Waziri wajaribu kuwa na rates za peak season na low season. Kwenye hoteli tayari tuna peak na low season na wakati huu mwezi Machi mpaka wa Julai pia airlines zina low season. Kwa hiyo, ningeshauri Wizara muangalie ni namna gani mnaweza mkapunguza ile park fee ili tuweze kuendana na utalii kama nchi nyingine zinavyofanya; kunakuwa na low season na high season. Kwa hiyo, ningeshauri wafanye hivyo ili tuweze kuongeza watalii zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania Tourist Board imetengewa 4.1 billion. Kwenye hii 4.1 billion wametoa 1.4 kwa ajili ya mishahara, ina maana wanabaki na 2.6 billion. Mheshimiwa Waziri amesema wataenda kutangaza CNN, BBC na matangazo mengine wataweka kwenye majarida na kadhalika. Hata hivyo, kwenye Hotuba ya Upinzani wamesema mwaka 2013/2014, walifanya maonesho kule Sunderland - UK na wanadaiwa karibu shilingi bilioni tano. Sasa sielewi kama hii 2.6 billion inaenda kulipa deni au lile deni linalipwa na nani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia vifungu vyote vya randama ya Maliasili na Utalii sijaona hili deni wanalipaje. Mheshimiwa Waziri hebu alete bajeti ambayo ina uhalisia, watakuja kumtumbua hapa, watasema hafanyi kazi lakini pesa hapewi. Kwa hiyo, nafikiri ni vizuri aandikie bajeti yenye uhalisia, aseme madeni ni haya na anahitaji pesa kiasi hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kidogo Mlima Kilimanjaro. National Parks zimeingiza shilingi bilioni 185, out of shilingi 185, Kilimanjaro National Park imeingiza shilingi bilioni 60, hizi ni fedha nyingi sana. Najua KINAPA wanajaribu kujenga madarasa na kadhalika lakini bado Halmashauri zinazouzunguka Mlima Kilimanjaro hazifaidiki na mapato yanayotokana na Mlima Kilimanjaro. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo kwenye migodi wanapata 0.3% ya pesa zinazotokana na mgodi, kwa nini isifanyike hivyo kwa Kilimanjaro? Shilingi bilioni 60 ukitoa 0.3% ni hela nyingi sana ambazo zingepewa Halmashauri wakaweza kufanya maendeleo yao wenyewe, wakatengeneza zahanati na madarasa. Mheshimiwa Waziri hata Mwanga ipo katika hizi Halmashauri ambazo zinafaidika na mapato ya Mlima Kilimanjaro, kwa hiyo, nategemea atalichukulia hili on a serious note. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mlima Kilimanjaro ni lazima Wizara ishirikiane na Wizara ya Mazingira, Mlima Kilimanjaro unaharibika. Wamejaribu kukusanya takataka kutoka Mlima Kilimanjaro lakini bado hazijakwisha. Kwa sababu wataalam wako hapa kule Mti Mkubwa kupitia Lemosho na kule Barafu, vyoo viko vitatu na vya shimo ambapo ma-porter, ma-guide na wageni, zaidi ya watu 300 wanatumia vyoo hivyo. Tumekuwa tukiongea hapa ndani ya Bunge hili kuna vyoo ambavyo vilitoka Ujerumani kwa ajili ya majaribio sijui mpaka sasa hivi vyoo vile vimeishia wapi? Naomba Mheshimiwa Waziri wakati anakuja kujumuisha atueleze vile vyoo mpaka sasa hivi vimeishia wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hilo linaenda sambamba na maji. Barafu, Mweka na Millenium Towers, hakuna maji. Kwa nini sasa KINAPA wasichukue maji kutoka Karanga waka-pump yakaja pale juu ili watalii waweze kuyatumia badala ya sasa hivi wanaenda kuzoa maji mbali na kuyaleta pale. Sasa hivi kule crater watu wana camp crater lakini Mheshimiwa Waziri crater hamna choo, watu wanalala kule halafu ndiyo wanapanda juu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watalii wanakuja zaidi ya mara 10 wanakuta mambo ni yaleyale business as usual. Kwa hiyo, naomba waangalie ni jinsi gani wataweza kutengeneza kule crater kuwe pasafi, ni pachafu sana.
Kwa hiyo, waangalie ni jinsi gani wataweza kutengeneza kule juu ili hawa tour leaders wanaorudi waweze kutuletea watalii kwa wingi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie Southern Circuit. Southern Circuit tunashindwa kuiuza kwa sababu miundombinu si mizuri. Tumekuwa tukizungumza mara nyingi, sasa Wizara hii na Wizara ya Miundombinu iangalie ni jinsi gani inaweza kutengeneza miundombinu ya kwenda Southern Circuit. Wawekezaji wanakuja wanataka wakajenge hoteli lakini wageni watafikaje huko, hoteli ni ghali sana. Kuna ndege moja inayoenda huko inaitwa Coastal Air lakini price yake ni sawa na mtu anayetoka hapa kwenda Europe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wazungu wengi wanaokuja Tanzania wana-save for years. Unakuta mtu ame-save almost five, six years ili aweze kuja Tanzania. Tukumbuke wageni wengi wanakuja kwa credit card, akifika hapa anajaribu kuangalia ni kwa jinsi gani anaweza ku-save aizungukie Tanzania yetu ilivyo nzuri lakini unakuta mara nyingi wanaishia kwenye Nothern Circuit kwa sababu ni cheaper, kuna hoteli nyingi lakini wanashindwa kwenda Southern Circuit kwa sababu ni too expensive.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Serikali muangalie ni kwa jinsi gani mnaweza kushirikiana na Wizara ya Miundombinu ili muweze kutengeneza hizo barabara ili wawekezaji waweze kuja kujenga hoteli kule na tuweze kuiuza kama tunavyoiuza Nothern Circuit. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kidogo huyu mjusi aliyeko huko Ujerumani. Kambi ya Upinzani imezungumza vizuri sana, ni fedha nyingi zinazopatikana kule Ujerumani. Euro 25 kwa watu 550 unaongelea karibu shilingi bilioni nne, sasa hivi sisi hatuhitaji hizo shilingi bilioni nne kweli?
Mheshimiwa mwenyekiti, ni kwa nini sasa msifanye arrangement aidha na sisi tupate percent yetu kama ikishindikana msafirisheni basi yule mjusi. Akiwekwa kwenye meli akawekwa pale Dar-es-Salaam ina maana watalii watakuja Dar-es-Salaam badala ya kwenda Ujerumani na sisi tutafaidika. Kuna vipesa vidogovidogo tunahangaikanavyo kwa ajili ya zahanati na kadhalika si vitapatikana pale! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nategemea sasa Mheshimiwa Waziri anavyokuja kutujibu atatueleza ana mkakati gani wa kuhakikisha kwamba yule dinosaur wanamsafirisha aje hapa. Katika Bunge hili yule mama wa Lindi mpaka tukamuita mama mjusi humu ndani, alikuwa anamzungumzia kweli lakini hakuna kilichofanyika mpaka leo. Ni mategemeo yangu sasa kwa wakati huu Mheshimiwa Waziri atakuja na majibu atueleze ana mikakati gani ya kuhakikisha mjusi yule anarudi Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachonisikitisha, mpaka sasa hivi hatuna Bodi ya TANAPA. Naomba Waziri anapokuja kujumuisha hapa hebu atueleze ni kitu gani au ni kwa nini wanashindwa kuunda Bodi ya TANAPA? Vitu vingi sana haviendi, tunalalamika hapa bila Bodi hawawezi kwenda kufanya chochote. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri aje atueleze ni lini ataunda Bodi ya TANAPA…
(MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uokoaji katika Mlima Kilimanjaro bado huduma ya uokoaji siyo nzuri. Gari halifiki kwenye high altitude na tunapoteza maisha ya watu huko mlimani, kwa nini TANAPA wasinunue helkopta ambayo inaweza kuokoa watu na wagonjwa kwenye high altitude? Hii inaweza kutumika kwenye park zote kwa ajili ya uokoaji pia kulinda majangili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake waliopo half mile katika Mlima Kilimanjaro wananyanyaswa sana, wanapigwa na askari wanaolinda msituni, wanafikia hata kubakwa. Ikumbukwe kuwa wao ndiyo wanaolinda mlima, wanatumika kuzima moto unapowaka, wanasaidia watu wasikate miti na pia watu hutumia njia ili kwenda nyumbani. Kuna kijana alipigwa risasi akielekea nyumbani kutoka Kibosho anaitwa Kiwale, je, kesi yake imefikia wapi? Copy nimempa Mheshimiwa Waziri kwa reference.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Umbwe route katika Mlima Kilimanjaro, route hii ni nzuri sana lakini Umbwe cave hakuna maji wala choo, watu wanajisaidia kwenye misitu, hii ni aibu wakati wageni wanalipa kuingia kwenye hifadhi, ni kwa nini wasifuatwe walipe forest fees na park fees wakati park ni moja?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine Umbwe route hakuna walinzi wa msituni na ukizingatia camp hii ipo karibu kabisa na Kibosho. Umbwe kwa wana vijiji ni rahisi watalii kuvamia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, route ya Old Moshi tayari Wizara ya Miundombinu imetenga fedha kwa ajili ya kutengeneza barabara kutoka Kiboriloni, Kikarara, Kidia, mpaka Tsuduni na njia hii ni fupi kufika Uhuru Peak, kuna water falls na vipepeo, sasa ni lini route hii itaanza kazi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na wimbi la wazungu wanaojitokeza ku-volunteers kuja kufanya kazi, lakini sasa hivi wanachokifanya wanafanya biashara ya utalii na wanawalaza wageni majumbani katika mitaa ya Moshi, Soweto Rau na kadhalika, wanatumia biashara ya mlima bila kulipa kodi, nashauri tour operaters wote kuwe ni lazima wapeleke TALA licence na tax clearance ili kuonyesha wanalipa kodi. Hii itafanya kodi nyingi kukusanywa na itakuwa ngumu kubakiza fedha nyingi Ulaya.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia. Pamoja na kuleta Mpango wa Maendeleo wa 2017/2018 napenda kujua ni kwa kiasi gani mpango wa 2016 uliweza kutekelezwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya uchumi kwa maelezo ya Waziri inaimarika, lakini kwa uhalisia hali ni mbaya katika sekta nyingi. Mfano benki nyingi za biashara mikopo imeshuka na riba ni kubwa hata vyombo vya habari vimenukuliwa vikisema hayo. Baadhi ya benki mfano CRDB imepata hasara ya shilingi bilioni mbili na zaidi. Wafanyabiashara wanashindwa kurudisha mikopo na wengi wao hawaagizi tena bidhaa kutoka nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata Serikali yenyewe kwa mwaka 2016 akiba ya fedha za kigeni ilifikia dola milioni 3,870.3 na hizi zinaweza kuagiza bidhaa nje kwa miezi minne. Je, baada ya miezi minne Serikali imejipangaje? Thamani ya Tanzanian shilling inazidi kushuka na deni la Taifa linazidi kukua, hii ni hatari sana kwa Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya viwanda; Serikali imekuwa ikiimba wimbo wa nchi itakuwa ya viwanda, je, kuanzia wakati wa kampeni hadi sasa ni viwanda vingapi vimeongezeka? Bila kuwa na umeme wa uhakika na kilimo cha kibiashara ili wazalishe, viwanda hivyo vitakuwa ni vya nini? Tulikuwa na kiwanda cha General Tyre Arusha kilichobinafsishwa na Serikali ikakichukua na imekuwa ikitoa ahadi zaidi ya miaka kumi kiwanda kitaanza kazi lakini mpaka leo hakuna uelekeo. Ikumbukwe kiwanda kile kilikuwa kinazalisha matairi bora na kutoa ajira nyingi na Serikali kupata mapato. Nilitegemea Serikali ingetueleza ina mpango gani na kiwanda kile.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Utalii; hii ni kati ya sekta inayochangia katika pato la Taifa kwa zaidi ya 17%, lakini kwa sasa Serikali inaelekea kwenda kuua kabisa utalii katika nchi yetu. Kitendo cha Serikali kuongeza VAT katika utalii ukizingatia tayari sekta hii ina zaidi ya kodi/leseni 31 zinazolipwa, utalii wetu umekuwa ni ghali sana. Sipingi kulipa kodi lakini tupandishe kwa taratibu. Baadhi ya nchi za Ulaya sheria zao huwezi kupandisha bei zaidi ya 10%. Hivi hawa tembo, simba, twiga na kadhalika kutoka Tanzania tumewaongezea thamani gani wawe na bei kubwa kuwaona kuliko wale waliopo nchi jirani ya Kenya ambao hawalipiwi kodi?
Mheshimiwa Naibu Spika, ningetaka kujua hivi Wizara ya Fedha inapoandaa Mpango ni kwa kiasi gani wanashirikiana katika mawazo ya kupanga hii mipango na Wizara nyingine? Hivi inapoanzisha viwanda ni kwa kiasi gani wameandaa wataalam, malighafi na kadhalika?
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba ku-declare kwamba mimi ni mdau wa utalii na nitaanza na suala zima la hali ya utalii nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyotambua, utalii ni kati ya sekta ambayo inachangia katika pato la Taifa kwa asilimia 17.5, lakini nasikitika na naona kwamba asilimia hizi zitapungua. Mheshimiwa Waziri wakati akijibu hoja tulivyokuwa tunachangia Kamati ya Bajeti alisema ongezeko la VAT halikuathiri wageni kuja nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mdau; wageni wengi waliokuja mwaka jana; VAT tuliipitisha hapa Bungeni mwezi wa Sita na Sheria ikaanza kutumika mwezi wa Saba; watalii wanatoka nchi mbalimbali wengi walikuwa wameshaanza kusafiri kuja nchini Tanzania, kwa hiyo walikuwa wamesha-book package zao. Kwa vyovyote vile mgeni anakuja mpaka hapa Tanzania amefika unamwambia kwenye package yako na kuongezea eighteen percent hawakubali. Sasa badala yake wale local tour operators ndio waliolipia zile fedha za zaidi na badala ya kuwasaidia Watanzania mmezidi kuwaumiza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningependa ili tuweze kupata figure halisia baada ya mwaka huu tujue ni watalii wangapi wamekuja. Kwa mfano compare Januari mwaka jana na Januari mwaka huu tuone ni watalii wangapi wamefika. Mimi nipo kwenye sekta hii na Januari mwaka huu sasa hivi mahoteli ni matupu hakuna wageni, tujiulize ni kwa nini hakuna wageni? Kule kilimanjaro huwa tuna-run Kilimanjaro marathon; Kilimanjaro marathon ni international inaleta wageni wengi sana hapa Tanzania. Baada ya kukimbia huwa wanapanda mlima, wanaenda safari na wanaenda kwenye beach tours; lakini mwaka huu wageni ni wachache, mahoteli bado hayajajaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba muangalie ni kwa nini wageni hawa hawaji tena Tanzania wanaenda nchi jirani, wanaenda Mombasa. Tuna wanafunzi huwa wanakuja Tanzania kama volunteers wale wanafunzi they are about sixteen to eighteen years old, wanakuja, wazazi wao wanajitolea, wanakuja kwa three weeks holiday; wazazi wanajitolea, wanachangisha fedha wanakuja wanasaidia kwenye kujenga mashule kupaka rangi na kadhalika, lakini hapa Tanzania tumekuwa tukiwachaji work permit ya dola mia tano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke wale wanafunzi wakija wanalipa visa fee ya Dola hamsini, bado wakikaa hapa kwa wiki mbili wanapanda mlima, wanaenda safari na wanaenda mpaka Zanzibar. Sasa wazazi wao wamejitolea kuja kutusaidia Watanzania lakini wanachajiwa dola mia tano kwa kuja kujitolea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali mliangalie hili kwa sababu tunapoteza wageni wetu. Mwaka huu nilikuwa na wageni zaidi ya mia saba lakini wote wame-cancel wanaenda Mombasa, tutapata wageni karibu hamsini tu. Naomba Serikali iliangalie hili tujaribu kuondoa ile permit visa ya dola 500 atleast mchaji reasonable price, labda hata kama dola mia moja hivi itakuwa ni fair, lakini dola mia tano ni nyingi sana tukumbuke na wale ni wanafunzi na wale wazazi wanakuja kutusaidia sisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tunaamini michezo ni afya na kama Bunge la Tanzania ningefurahi sana tarehe 26 mwezi wa Pili kuwaalika Wabunge na nyie mje mkashiriki kwenye Kili Marathoni; mnaweza mkakimbia zile kilomita tano kama sapoti kwa sababu zile ni fun run mnaweza mkatembea ama mkakimbia, lakini itakuwa na sisi kama Watanzania tumeonesha moyo katika haya mashindano ya Kimataifa ambayo watu wanatoka all over the world lakini sisi kama Watanzania na kama Bunge la Tanzania bado wengi wetu hatujaweza kwenda katika mashindano yale.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Mgogoro wa ongezeko la vijiji kuingia hifadhi, Mbarali Mbeya. TANAPA inaongoza vijiji 21 kuingia katika hifadhi lakini vijiji hivi ni vya wakulima wa mpunga na mgogoro huu umekuwepo kwa
zaidi ya miaka nane. Wakati wa kampeni za Urais 2015 Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli aliahidi kuwatengenezea barabara ya lami ambayo imeanza kutekelezwa na akatoa agizo vijiji vile visichukuliwe na hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima hawa wa mpunga wanazalisha magunia mpaka 1,300,000 sawa na tani 104,000 kwa mwaka. Katika vijiji hivyo vipo viwanda vya kukoboa mpunga vikubwa 42 na magodauni 56 makubwa. Kwa kuvichukua vijiji hivi tayari ajira zitapotea takriban watu 10,000 watakosa ajira. Ukizingatia agizo la Rais ni kuwa Tanzania ya viwanda. Je kwa kutaifisha vijiji hivi na kuvifanya hifadhi Tanzania ya viwanda itatekelezekaje? Serikali isitishe kuvichukua vijiji 21 kwa faida ya maendeleo ya wananchi wanaoishi pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, michezo ni afya na kwa sasa hivi magonjwa yasiyoambukiza kama sukari ya kupanda na kushuka na shinikizo la damu la kupanda na kushuka magonjwa ya moyo magonjwa haya kwa sasa yanawapata hasa watoto wadogo lakini yanaweza kuzuilika kwa watu kufanya mazoezi na Serikali kupitia Makamu wa Rais, aliagiza watu wafanye mazoezi kwa nia nzuri tu lakini cha kujiuliza watu watafanyia wapi mazoezi. Halmashauri nyingi hazina viwanja vya michezo na Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hotuba yake hajaelezea kabisa mikakati ya kujenga viwanja na ya kupata viwanja hivyo vya mazoezi?
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia. Mimi nitachangia katika suala zima la UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa zinaonesha kwamba UKIMWI bado maambukizi yapo nami ninaona kama ni janga la Taifa. Watu zaidi ya milioni 1.4 sasa hivi wameambukizwa HIV na watu 54,000 wana maambukizi mapya na watu 36,000 wamekufa na AIDS, asilimia 53 wanatumia dawa za ARV. Takwimu hizi zinatisha, lakini kitu kinachonisikitisha, Mfuko wa UKIMWI bado haujatoa fedha za kutosha. Zamani tuliona kwamba waliweza kutoa matangazo, kuweka vibao kwa ajili ya kutoa elimu kwa ajili ya UKIMWI, lakini sasa hivi matangazo yale hayapo na tumeona mara nyingi nimekuwa nikizungumzia suala zima la maambukizi ya UKIMWI kutokana na wanawake wanavyoenda saluni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake huwa wanakwenda saluni kutengeneza kucha na wakitengeneza kucha wana-share vile vyombo, zile nail cutters kwa ajili ya kusafishia kucha. Ni hatari sana sababu vyombo vile havisafishwi ni chuma na huwa saa nyingine mtu anaweza akajitoboa na kuambukiza yule ambaye alikuwa ameenda saluni kutengeneza kucha. Sijui ni kwa jinsi gani mpaka leo hii Wizara imeweza kuwapelekea wale wenye saluni elimu hii ili waweze kutumia vifaa vya kinga, maana saa nyingine wanafanya hata scrub, anaweza akam-scrub yule mtu lakini yule mtu ukute ana kidonda au yule anayefanya ile scrubing na yeye ana kidonda, kwa namna moja au nyingine anamuambukiza yule ambaye alikuwa anamfanyia hiyo scrubing.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hizi treatment centre, unakuta watu wenye UKIMWI wanaenda sehemu moja kwenye kitengo ambacho wanakwenda kupata ushauri nasaha pamoja na kupewa dawa, lakini wamekuwa wanapata unyanyapaa na unyanyapaa bado unaendelea. Mimi ningeshauri, ni kwa jinsi gani Serikali inaweza ikajumlisha magonjwa sugu kama kisukari, shinikizo la damu na hawa wenye magonjwa ya UKIMWI wakakaa pamoja, wakapewa zile treatment, wakapewa dawa na hii itawafanya wale wagonjwa wenye UKIMWI kuwa na ari zaidi ya kuweza kwenda kupimwa na wale ambao wana magonjwa ya kisukari na magonjwa ya shinikizo la damu wataweza kukubali kupimwa kwa urahisi kwa sababu watajisikia kwamba hawanyanyapaliwi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo hii inaenda sambamba na dawa za kulevya na viroba. Hivi ni vitu ambavyo vinapunguza sana nguvu kazi katika nchi yetu, vijana wengi sana wameathirika, tunajaribu kujenga shule lakini sijui hawa watoto watakaokwenda kwenye hizo shule ni nani kama hatutalichukulia janga hili kama janga la Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha vijana zaidi ya 550,000 wameathirika na dawa za kulevya . Kati ya hao 550,000 ni 50,000 ni kwa ajili ya kujidunga zile sindano na tunajua kabisa wakijidunga sindano wanaweza wakapata maambukizi ya UKIMWI. Mimi nafikiri Serikali ingewachukulia hawa mateja kama wagonjwa badala ya kuwakamata na kwenda kuwafunga lock up. Hawa ni watu ambao wanahitaji kutibiwa kwa sababu ni wagonjwa na mara nyingi hawa mateja badala ya kuwapeleka hospitali za watu wenye magonjwa ya akili, mimi nashauri mtengeneze centres za kuwapeleka hawa vijana kwa sababau vijana hawa siyo vichaa, unakuta tu wamekuwa mazombi fulani wala hawamdhuru mtu lakini ukienda kuwachanganya na wale wagonjwa wenye matatizo ya akili wale wanakuwa hyper wanaweza wakawapiga, wanachukua vyuma wanapiga watu, lakini hawa wanahitaji kwamba wawekwe mahali vizuri, wapewe dawa, wapewe elimu ili waweze kuondokana na dawa za kulevya .
Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na wenzangu wote kabisa hii habari ya kukamata vijana ambao wanatumia dawa za kulevya wale ni innocent, wanatumia tu zile dawa mimi nafikiri ni vizuri mkawakamata wale wanao-supply na hawa vijana wapelekwe waende wakatibiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka haraka naomba nizungumzie suala zima la saratani; Saratani tunajua kutokana na taarifa ni zaidi ya watu 27,000 wanafariki kwa ajili ya magonjwa ya saratani. Kuna baadhi ya saratani kama elimu ikitolewa ya kutosha yanaweza yakatibika, kama tezi dume, saratani ya shingo ya kizazi, saratani ya matiti inayotokana na ulaji mwingi wa mafuta, kuna Saratani nyingine za ngozi ambazo wanawake wanatumia vipodozi vya kujichubua wanapata ugonjwa wa kansa kutokana na vipodozi. Wizara itoe elimu, wanawake waache kutumia hivi vipodozi vya kemikali kali ili...
(Hapa kengele ililia kuashiri kwisha kwa muda wa Mzungumzaji )
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Utunzaji wa mazingira ni muhimu sana katika kuleta maendeleo, kuleta hewa safi, kuongeza mvua na kadhalika. Sisi wote ni mashahidi katika nchi yetu, kumekuwepo na ukame wa kupitiliza kiasi hata mazao hayawezi kulimwa, vyanzo vya maji vinakauka na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri, Serikali kwa kupitia kila Kitongoji na Kijiji zile Kamati za Mazingira ziimarishwe, ziwezeshwe kama ilivyokuwa miaka 30 iliyopita. Ilikuwa ni lazima kupanda miti kila shule kuwa na vitalu vya miche, mfano Kilimanjaro ilikuwa hairuhusiwi kulima au kujenga kandokando mwa mto na mifereji iliyokuwa inatiririka maji na mito lakini sasa hivi yote imekauka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuyeyuka kwa theluji ya mlima Kilimanjaro, miaka ya hivi karibuni Profesa L. Thomson kutoka University ya Ohio kule Marekani walikuja kufanya utafiti ni kwa nini theluji inapungua kwenye mlima Kilimanjaro, walibeba barafu nyingi sana (in tons) kuzipeleka Marekani. Je, Serikali mmefuatilia walibaini ni kwa nini theluji inapungua katika mlima Kilimanjaro?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tukisubiri sababu ni vizuri kuhimiza miti kupandwa kwa wingi ili wananchi waweze kupata maji na mvua, kwa sasa hivi Mji wa Moshi ndio wenye joto kubwa kuliko popote hapa nchini na Moshi ipo chini ya Mlima Kilimanjaro hii ni hali ya hatari sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukataji wa miti kwa ajili ya mkaa, ni vizuri Wizara hii na Wizara ya Nishati na Madini waangalie ni jinsi gani wanaweza kushusha bei ya gesi ya kupikia ili kila mwananchi aweze kununua gesi ya kupikia. Hii itasaidia kupunguza uharibifu wa mazingira, miti haitakatwa kwa sababu ya mkaa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Ucheleweshwaji wa kusikiliza kesi za mahabusu. Baada ya kesi zilizopo katika uchunguzi chini ya DPP zinachukua muda mrefu sana na wakati watuhumiwa wengine hawana hatia lakini wanaweza kuwa gerezani kwa zaidi ya miezi sita. Je, kesi hizi hazina kikomo cha uchunguzi? Inakuwa kama wanakomoa na kudhalilisha wengine na huu ni ukiukwaji wa haki za binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya Mfuko wa Mahakama, bado mfuko huu wa fedha zinazoainishwa hazifiki kwa wakati na hata wakizipata zinakuja zimechelewa na pungufu ambayo inakuwa ni vigumu kutekeleza miradi ya maendeleo hii inajionesha mpaka Machi 2017, fedha hazikutumwa kwa wakati. Chombo hiki ni muhimu sana nashauri fedha zipelekwe kwa wakati ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wapo watumishi wa kutosha, kuhakikisha posho za wazee wa mabaraza zinalipwa, wazee hawa wanaacha shughuli zao wengine inabidi watumie nauli zao, hivyo, wana haki ya kupata stahili zao kwa wakati.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia. Barabara ya Morogoro kuanzia Mlandizi mpaka Chalinze; barabara hii imekuwa ikikarabatiwa mara kwa mara, lakini bado barabara hii haipo katika kiwango chake kwa kisingizio kwamba water table ipo juu, ni kwa nini wataalam wasifanye utafiti na kuijenga kwa kisasa. Nchi zilizoendelea wanajenga mpaka juu ya bahari hapa Tanzania shida ni nini? Je, Mkandarasi huwa hatoi guarantee ni muda gani barabara itadumu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Old - Moshi iliyopo Moshi kuanzia Kiboriloni- Kikarara – Kidia hadi Tsuduni, hii ni kati ya barabara iliyokuwa katika ahadi ya Mheshimiwa Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete katika kampeni za Urais 2010 na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli wakati huo alikuwa Waziri wa Ujenzi na katika Bunge hili Tukufu kwenye hotuba yake ya bajeti 2016, aliahidi kutenga fedha kwa ajili ya barabara teule na si hivyo tu, niliuliza swali mwaka huu na nikajibiwa upembuzi yakinifu umekamilika na walikuwa kwenye mchakato wa kumtafuta Mkandarasi. Je, ni muda gani unaotumika kumpata Mkandarasi. Je, barabara hii ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami ukizingatia barabara hii ni muhimu sana na maendeleo ya uchumi wa nchi yetu kwenye sekta ya utalii. Sababu ni njia fupi sana ya kufika kilele cha Mlima Kilimanjaro na ina vivutio kama vipepeo na ndege wengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja wa Ndege wa Moshi, uwanja huu umesahaulika kwa muda mrefu hata barabara ya kuelekea airport imefunikwa na majani, wananchi wanalima mazao katika eneo la airport. Uwanja huu ni very strategic kwa ajili ya watalii kuja moja kwa moja
kupitia nchi jirani. Serikali imekuwa ikiahidi watakarabati kiwanja kile, je, ni lini wataanza kukikarabati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Moshi maeneo ya Kiboriloni KDC kumekuwepo na matatizo ya mawasiliano sasa licha ya kuwa karibu na Mjini na suala hili limeshapelekwa kwa mitandao yote ya simu, lakini hakuna kinachotendeka. Je, ni lini Serikali itatusaidia minara ya simu iwekwe pale KDC, Mbokomu ili wananchi wa pale waweze kupata mawasiliano.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia. Nianze na utamaduni. Palikuwepo na mchakato wa kuanzisha vazi la Taifa na fedha zilitumika katika mchakato wa kupata vazi hili ilifikia mpaka kutolewa mifano ya vazi la Taifa. Je, mchakato ule umefikia wapi na mpaka sasa fedha kiasi gani zimetumika?

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi vijana wetu maadili yameporomoka sana, kuanzia mavazi hata baadhi ya lugha wanazotumia, heshima kwa wakubwa hakuna na kupoteza kabisa mila na desturi ya Watanzania ya kuheshimu hata wakubwa zao. Je, Serikali imejipangaje kurudisha maadili na utamaduni wetu wa Kitanzania wa kuheshimiana? Tukiimarisha utamaduni wetu, wa kucheza ngoma za kienyeji, mapishi ya kienyeji na kadhalika inaweza kuwa ni moja ya vivutio vya utalii hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, michezo. Kutokana na magonjwa kuongezeka duniani magonjwa yasiyoambukiza kama sukari ya kupanda, shinikizo la damu la kupanda juu na magonjwa ya moyo, mazoezi ya mara kwa mara yanaweza kupunguza magonjwa haya. Je, Serikali wamejiandaa kwa kiasi gani kuhakikisha wanajenga viwanja vya michezo kwa Wilaya kwa kuanzia lakini ziteremke chini kila Halmashauri?

Mheshimiwa Spika, kiwanja cha King Memorial kilichopo Manispaa ya Moshi. Uwanja huu ni mkubwa kabisa na michezo zaidi ya saba. Hakuna uwanja Moshi na uwanja huu ni wa Mkoa. Tumekuwa tukitumia uwanja wa ushirika ambao ni mdogo, tulishuhudia sherehe za Mei Mosi 2017 pale uwanja wa Ushirika walishindwa kufanya maonesho ya magari kwa sababu ya udogo wa uwanja. Hata mashindano yajulikanayo kama Kilimanjaro marathon huwa yanafanyika uwanja wa Ushirika, lakini michezo hii imekuwa sana inaleta wageni duniani pote kwa sasa ni padogo na suluhisho ni kuutengeneza uwanja wa King Memorial. Hivi inaingia akilini King Memorial penye heka zaidi ya 10 patumike tu kama soko la kuuzia mitumba ambayo hawatumii hata eneo lisilozidi heka mbili? Kwa nini wasipatiwe sehemu nyingine kama kule Pasua, Manyema na kadhalika, sehemu zipo nyingi.

Mheshimiwa Spika, habari. Ni haki ya Watanzania kupata habari. Hii ikiwa ni pamoja na wananchi hawa kupata habari zinazoendelea Bungeni ili wajue Wabunge wao kama wanawasilisha matatizo yao. Kwa kuwanyima haki hii ni uvunjifu wa Katiba. Je, ni lini shughuli zote za Bunge zitarudishwa na kuanza kurushwa live ili wananchi waweze kupata habari kuhusu nini kinaendelea Bungeni? Kwa nini Serikali inaogopa?
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugonjwa wa saratani kwa sasa hivi katika dunia ni ugonjwa hatari sana pamoja na saratani ya shingo ya kizazi imekuwa ni tishio. Zaidi ya wanawake 274,000 duniani wanafariki kwa ugonjwa huu na Tanzania ikiwa ni mojawapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru hospitali ya Ocean Road imekuwa ikitoa huduma ya mionzi na kusaidia wagonjwa wa saratani lakini hospitali ile wote tunashuhudia imezidiwa na wagonjwa ni wengi. Nashukuru hospitali ya rufaa KCMC ilipata wafadhili na wakafadhili jengo kwa ajili ya unit ya kansa, walijenga kwa shilingi bilioni 1.2 na wafadhili kwa sasa hivi wako tayari kununua vifaa kwa ajili ya mionzi, kutoa vifaa zaidi ya shilingi bilioni sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, kwenye kitabu cha maendeleo umetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya KCMC, jengo ambalo ni special kwa kitaalam linaitwa banker linahitajika kwa ajili ya kuweka vile vifaa vya mionzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, KCMC tunachoomba, Serikali itusaidie wanahitaji shilingi bilioni saba. Tunamwomba Waziri wa Fedha na Kamati yako ya Bajeti mkae chini muangalie ni kwa jinsi gani mnaweza mkaipatia KCMC hizi shilingi bilioni saba ili waweze kujenga lile jengo. Kwa sababu, Kanda ya Kaskazini itapunguza msongamano katika Hospitali ya Ocean Road, inaweza ika-save zaidi watu milioni 15 na kwa kiasi kikubwa tunaweza tukapunguza ugonjwa wa saratani ya kizazi kwa wanawake na kutoa huduma ya mionzi pale KCMC.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kidogo magonjwa yasiyoambukiza (non-communicable disease). Nimekuwa nikiongea mara nyingi hapa, ninamshukuru Mheshimiwa Waziri amesema wameanzisha watu kwenda mazoezi na kadhalika, nafikiri ni vizuri sasa Wizara hizi zikashirikiana Wizara ya Miundombinu na Michezo ili muweze kujenga pavement kwa ajili ya watu kutembea kwa miguu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia pale Dar es Salaam kwa mfano, zile njia ya majitaka (sewage system) mnaweza mkazifunika na watu wakaweza kupita kwa miguu. Nchi zilizoendelea kwa sasa hivi wanahimiza watu waende kazini kwa kutumia baiskeli, kwa sehemu kama Dar es Salaam mtu atatembeaje na baiskeli? Kutembea tu kwa miguu unagongwa na bodaboda. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali mkashirikiana kwa pamoja mkatengeneza pavement kwa ajili ya watu wa kutembea kwa miguu na kwa kiasi kikubwa sana tutapunguza magonja ya kisukari ambayo inasemekana Tanzania watu zaidi ya asilimia tisa wana ugonjwa wa kisukari mpaka watoto wadogo wana wanapata kisukari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zilizoendelea wameacha kabisa ku-serve hivi vyakula vya junk food, lakini sasa hivi ndiyo vimeanza kuletwa Tanzania kama Kentucky, Fried Chicken na kadhalika. Ni vizuri mkazidi kutupa elimu ili watu waachane na hivyo vyakula ambavyo vinaongeza magonjwa ya shinikizo la damu ya kupanda na kushuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kidogo nizungumzie mimba za utotoni. Mimba za utotoni imekuwa ni hatari kwa kweli. Pamoja na kusema watoto wadogo wanaweza kuolewa chini ya miaka 18 mimi napinga jambo hili, kwa sababu kwanza tunawakosesha watoto wale elimu, pili mtoto wa kike akijifungua kabla ya umri wake anaweza akapata magonjwa kama ya fistula, tatu anaweza kushindwa kujifungua inabidi atumie scissor na wengine baada ya hapo wanakuwa ni single parent, unakuta wazazi wenyewe wakati mwingine wana wanyanyapaa wanawaambia hukusoma, kwa hiyo watoto wale wanaishia kuwa watoto wa mtaani, wanashindwa kuendelea na masomo, wanaweza kwenda kuwa machangudoa na hii ni kumrudisha mtoto wa kike nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna moja au nyingine naomba Wabunge tukubaliane na hili, tuliona wenyewe juzi tulivyoongelea suala hili, Sheria ile ya Ndoa ya mwaka 1971 ibadilishwe wengine walikuwa wanapinga kutokana na imani zao za dini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Upinzani naomba muichukue na muifanyie kazi kwa sababu ina ushauri wa kutokasha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kuhusu nyumba za walimu. Sehemu za vijijini pamezidi kuwa na uhaba wa walimu, unakuta shule moja ina walimu wawili tu. Tatizo hili linatokana na kwamba unakuta mwalimu ametoka nyumbani kwake kwenye mahitaji yote anapangiwa shule za vijijini anakuta hakuna nyumba za walimu hata zikiwepo ni nyumba zisizokuwa na mahitaji yote jambo linalopelekea walimu wengi kukata tamaa kwenda vijijini sababu ya tatizo hilo. Nyumba za wakazi huwa mbali sana na shule. Je, Serikali ina mpango gani wa kupambana na changamoto hii ya uhaba wa makazi ya walimu? Sababu mwalimu asipopata makazi mazuri hatakuwa na morali ya kufundisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni madai ya walimu. Suala hili limekuwa ni jambo la kawaida kwa walimu kutolipwa stahiki zao kwa wakati. Kila mara tumeshuhudia walimu wakienda kudai fedha zao hawalipwi na madeni kuzidi kuwa makubwa. Tatizo lipo kwa walimu waliopo kazini na wakistaafu bado wananyanyaswa. Zaidi ya wastaafu 1,000 wanadai shilingi bilioni 138 ambazo ni mafao ya michango yao kwa NSSF na PSPF. Je, Serikali ina mikakati gani ya kutenga fedha kwa ajili ya wastaafu hawa?

Tatu, ni kuhusu wanafunzi wa kike wanaopata ujauzito wakiwa bado masomoni. Pamoja na kutenda kosa hilo lakini mtoto wa kike anaadhibiwa kwa kutoendelea na masomo wakati unakuta pengine aliyempa ujauzito wapo shule moja na anaendelea na masomo. Ni vizuri Serikali iliangalie suala hili kwa kuwaruhusu kuja kuendelea na masomo yao baada ya kujifungua lakini kuwe na special school kwa ajili yao ili wenzao wasije wakawanyanyapaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ni kuhusu vyeti vya kughushi. Zoezi hili limewaathiri wafanyakazi wengi hadi kupelekea wengine kupata mishtuko ya moyo. Ni vizuri zoezi hili lingepangwa kwa madaraja, kuna wale walioghushi cheti kabisa, lakini kuna wale wametumia cha ndugu yake aliyeshindwa kuendelea kutoka darasa la saba na akaendelea kusoma na kufauli mpaka akapata Ph.D. Aidha, mtu huyu unakuta amefanya kazi kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kama naunga mkono kutumia vyeti fake, lakini naisihi Serikali iwe na jicho la huruma kuwasamehe na kuwalipa mafao yao. Kama Serikali iliweza kuwasamehe mafisadi wa EPA iweje ishindwe kuwasamehe hawa? Kwa nini Serikali iliifumbia macho dhambi hii ya kutumia vyeti fake na wahusika walioajiri watu hawa wamewajibishwa vipi?

Nashauri kwa wale wanaolalamika wameonewa basi Serikali ifungue milango kwa watu hawa kwenda kulalamika na Serikali iwastaafishe kwa manufaa ya umma na walipwe posho zao zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwa na vyeti fake pia kuna elimu fake. Unakuta mtoto anaingia kidato cha kwanza hajui kusoma, kuandika wala kuhesabu. Kuna vitabu vya kufundishia vinachapwa na makosa tunategemea nini katika elimu ya watoto hawa?
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Ili mtu aweze kuendelea ni lazima kwanza awe na afya bora. Hivyo basi, sekta ya afya ni muhimu sana kuhakikisha Serikali inatenga bajeti ya kutosha. Je, ni lini Serikali itatimiza Azimio la Abuja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu magonjwa yasiyoambukizwa None Communicable Diseases(NCD); magonjwa haya kama sukari ya kupanda na kushuka, shinikizo la damu ya kupanda na kushuka, magonjwa ya moyo na kadhalika, mengi ya magonjwa hapa yanayoweza kuepukika tu kama elimu ya kutosha inaweza kutolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, siku hizi imekuwa ni kawaida watu kununua vyakula vya barabarani kama chips, mihogo, sambusa na juice zenye sukari nyingi, unywaji wa pombe na ulaji wa nyama nyekundu kupita kiasi, vitu vyote hivi vinachangia kuongezeka kwa magonjwa haya, hata watoto wadogo mpaka wenye miaka 10 wanapata magonjwa haya. Je, Serikali ina mikakati gani ya kupunguza au kutokomeza magonjwa haya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano nchi za Ulaya sasa hivi wanahimiza watu kufanya mazoezi, wanashauri wafanyakazi kutembea kwenda kazini, lakini hapa kwetu ni vigumu sababu barabara zetu siyo rafiki kwa matembezi ya miguu. Ni kwa nini Wizara ya Afya isishirikiane na Wizara ya Miundombinu ili wakijenga barabara wahakikishe wanajenga barabara za wapita kwa miguu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ndoa za utotoni na mimba za utotoni. Ni wakati muafaka sasa kuhakikisha Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 inarekebishwe ili isiruhusu watoto wa kike kuolewa wakiwa na miaka 14, tukumbuke wasichana hawa wakipata mimba utotoni mara nyingi wakati wa kujifungua huchukua muda mrefu sababu uchungu huchukua muda mrefu na hali hii huweza kusababisha kifo cha mama au mtoto au wote wawili kama matibabu ya dharura ya upasuaji kwa ajili ya uzazi hayatafanyika na ukizingatia vijijini huduma hizi sehemu nyingi hazipo na umbali wa kutoka kijijini mpaka Wilayani miundombinu ni mibovu pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto hawa pia hukosa fursa ya elimu kwa kuwa wengi wao hufukuzwa shule, wazazi husita kuwaendeleza na hii hupelekea baadhi ya watoto hawa wa kike kufungua mlango wa kuingia katika umaskini na kuzaa ovyo bila mpangilio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa zaidi wengi hupata fistula (vescovaginal fistula (VVF) au rectovagina fistula (RUF), hii husababisha msichana kutokwa na haja ndogo au kubwa bila kujizuia. Haja kubwa pia inaweza kumtoka msichana kwa kupitia tupu ya mbele na hii kuharibu sana afya ya mwili na hisia za msichana. Hayo ni machache tu kati ya matatizo ya mimba za utotoni, ni imani yangu Serikali itayaona haya na kuleta marekebisho ya sheria mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa vifaa tiba na madawa. Hospitali nyingi hazina vifaa vya akina mama vya kujifungulia, hata baadhi ya hospitali hazina madawa. Mfano, tarehe 28 Februari, 2017 kulikuwa na mashindano ya Kilimanjaro Marathon na pale uwanjani kulikuwa na kitengo cha huduma ya kwanza, jambo la kusikitisha pale kwenye huduma ya kwanza hawakuwa na mtungi wa kuongeza hewa (oxygen). alikuwa na kijana aliyekimbia na alikuwa mahututi na alihitaji oxygen lakini wahudumu wale hawakuwa na mtungi wa oxygen na kibaya zaidi ambulance ilivyofika na wao pia hawakuwa na oxygen cylinder na kupelekea kijana yule kufariki pale uwanjani. Mungu alilaze roho yake mahali pema peponi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama magari yote ya kuokoa yangekuwepo na vifaa vyote, pengine kijana yule angeweza kupona. Je, katika bajeti hii ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya vifaa hivi hata MRI kwa ajili ya Hospitali ya Rufaa ya KCMC? Kipimo hiki ni muhimu sana kwa Hospitali ya Rufaa kutokuwa nacho unakuta wagonjwa wanaagiziwa kwenda kwenye hospitiali za binafsi kufanya vipimo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Hospitali ya KCMC kwa kuanzisha kitengo cha saratani kama ilivyo Ocean Road, ni vizuri kitengo hiki kianzishwe Mwanza na Mbeya. Serikali iwasaidie kwa kupeleka wataalam, vifaa tiba na ruzuku kwa ajili ya kitengo cha kansa kule KCMC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi milioni 500 hazitoshi zinahitajika shilingi bilioni saba za kujenga jengo la kuweka vifaa walivyovipata vya msaada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamekuwepo na ongezeko kubwa sana la kansa ya shingo ya kizazi, tumepoteza akina mama wengi lakini ugonjwa huu unaweza kuepukika kama ukigundulika mapema, lakini huduma ya kansa ya kizazi sio hospitali zote zinatoa huduma hapa nchini na kupelekea vifo vingi. Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka huduma hizi hata mpaka kwenye ngazi ya vituo vya afya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado maambukizi ya UKIMWI yapo juu sana, lakini kuna tatizo kubwa la upatikanaji wa kondomu za kike, je, Serikali ina mpango gani ili tuokoe watoto wa kike?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyozungumza utalii unachangia sana katika pato la Taifa, lakini wafanyabiashara katika sekta hii, niungane na wenzangu kusema kwamba tozo na kodi ni nyingi sana, ziko kodi 36 na nimeziambatanisha hapa naomba uzione ili wakati Kamati ya Bajeti inakaa wakati wa Finance Bill waangalie ni jinsi gani wanaweza wakazipunguza kodi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anasema kwamba VAT haikuathiri watalii kuja nchini. Kwa mfano kabla ya VAT Ngorongoro Crater mwaka 2014 walikuja watalii 332,163, mwaka 2016 wamekuja watalii kuingia Crater 228,689, kuna pungufu ya 103,000, sasa kama wanabisha siyo VAT, basi wafanye uchunguzi ni kitu gani kinafanya watalii hawaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuko katika sekta, watalii wengi walikataa kulipa zile VAT. Sasa wao wanasema watalii wameongezeka sijui hizi takwimu wanatoa wapi, sijui mnajumlishia na hao Wachina wanaokuja kujenga barabara huku, sielewi kwa kweli, naomba Waziri atueleze hizi takwimu anazitoa wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kodi nyingi sekta hii inakuwa vigumu sana kufanya matangazo, unakuta wafanyabiashara wana kodi nyingi lakini ni wao wao watengeneze vipeperushi, wajilipie exhibition lakini TTB haiwezeshwi. TTB mwaka 2016 waliomba shilingi bilioni 2.7 mpaka sasa hivi wamepata milioni 422, watafanyaje advertisements?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kuna masoko mapya kama Nchi za Czech, Ukraine, Yugoslavia na sehemu nyinginezo, wanataka kuja Tanzania lakini TTB ndiyo inayotakiwa iende ikatangaze vivutio vya Tanzania lakini wanashindwa, kuna vivutio vingi. Mathalani, Mkoa wa Kilimanjaro Kijiji cha Mrusunga, Kata ya Mbokomu, Moshi Vijijini, kuna mti mrefu mita 80 mti ule unakadiriwa umekaa zaidi ya miaka 500, lakini Wizara ya Utalii haijafanya utafiti wowote, wanatakiwa waende wakaweke uzio pale ili muuweke kati ya vivutio wageni wanavyokuja kutembelea Mlima Kilimanjaro, wakati wanangojea kupanda, wakati wa climatization, tuiweke kwenye itinerary Wazungu waweze kwenda pale waende wakapige picha na tunaweza kupata mapato. Wizara imekaa kimya sijui wanasubiri mzungu aje apige picha aseme ame-discover mti mrefu Afrika, wakati watafiti wako hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri hivi vitu tuvifanye wenyewe na tuwe proud na nchi yetu wenyewe, tusingojee Wazungu waje hapa watuambie wame- discover Mlima Kilimanjaro wakati sisi tuko hapa na babu zetu walikuwa wanaokota kuni kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la wakulima na hifadhi TANAPA. Mfano, kuna wakulima wanaolima mpunga kule Mbarali wakulima hao wana vijiji 32, TANAPA inataka iende ikachukue vijiji vile ifanye hifadhi, lakini wameshaendelea wamejenga viwanda zaidi ya 46 wana ma-godown karibu 56, wana wafanyakazi zaidi ya 10,000, viwanda vile walivijenga kwa zaidi ya billioni 72, tayari wameshawekeza kwenye viwanda na Serikali wanasema Tanzania ya viwanda, sasa hivi wanataka kwenda kuwanyang’anya vile viwanda, sasa wataenda wapi, watafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri nimeshazungumza naye na pia nilimwona Waziri Mkuu kuhusiana na suala hili. Naomba vile vijiji waviache waendelee na ile kazi tayari ni ajira iko pale, tayari viwanda viko pale, wawaache wafanye kazi, waende wakaendeleze hifadhi nyingine. Kuna hifadhi kama ya Selous inatakiwa kuendelezwa, Saadani inatakiwa kuendelezwa, sasa wanaenda kufukuza watu ambao tayari wana makazi, wana wafanyakazi, wana kila kitu, kwa nini wasiende huko ambako kunatakiwa kuendelezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa nimekosea sana kama sitauongelea Mlima Kilimanjaro. Kila siku nimekuwa katika Bunge hili tangu tumeanza naongelea suala la rescue.

Rescue katika Mlima Kilimanjaro bado hairidhishi, unakuta mgonjwa anaugua kule juu, sijui ni kwa nini pamoja na mapato yote haya wanayopata kutoka Mlima Kilimanjaro wasinunue helicopter ya ku-rescue wagonjwa wanaopata matatizo kule mlimani ikiwa ni pamoja na ma-porter.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni shida mtu akipata ugonjwa kutoka Uhuru Peak mpaka ashushwe chini, akutane na gari ya National Park ile inayo-rescue unakuta ameshakufa, ni zaidi ya masaa kumi, lakini wakinunua helicopter yenye uwezo wa kuweza kushuka kule Shira wataokoa maisha ya watu na wale Wazungu wanaokuja wataona kwamba tunawajali pamoja na Porters, lakini sisi tumekuwa tukiwaleta kwa mikono, wanakufa, wanaenda kufanya uchunguzi kwa nini wamekufa lakini tatizo ni rescue system tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo nimeulizia mara nyingi kuhusu vyoo, vyoo ni tatizo katika mlima wetu mmesema watu wanaenda ku-camp crater naomba kumuuliza Mheshimwa Waziri wana-camp crater watajisaidia wapi? Mazingira tutayatunzaje? pale crater hamna choo, vile vyoo vilivyoko kwenye camping roots ni vya shimo, vimejaa, kila Tour Operator anajaribu kupeleka chemical portable toilets, lakini ile waste wanaipeleka wapi? Wanaenda kuimwaga kule kwenye yale mashimo ya National Park ya choo, lakini bado yamejaa, kwa hiyo bado yale mazingira Mlima unarudi pale pale kunazidi kuwa kuchafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naomba sana, hili suala la choo, kuna vile vyoo vya Wajerumani mlivyovileta vya kujaribu vimeishia wapi? Maana yake mnakuja hapa mnaongea maneno mazuri lakini hamtekelezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine tunacholalamika kule Kilimanjaro ni fees za forest. Mtu analipa National park fee mfano kule Umbwe, Longai na Lemosho, unalipa forest fee unalipa na National Park fee, unaenda mpaka Umbwe unafika Umbwe hakuna maji, inabidi warudi tena chini wanunue tena maji, zote hizi ni tozo tu zinazidi sasa unakuta tunashindwa kufanya biashara kwa sababu ya hivi vitozo vidogovidogo. Kwa hiyo, naomba sana waliangalie hilo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine pamoja na mambo mengine ni lile suala la Faru Fausta, Faru Fausta anatumia fedha nyingi sana shilingi millioni 60 kwa mwezi ni fedha nyingi. Mnyama yule alizoea kutembea huru, hivi kwa nini msimuache afe naturaly kama anavyokufa tembo, anavyokufa simba lakini anakuwa ni chakula kwa ajili ya wale wanyama wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini wanamtesa yule mnyama wanamfungia kwenye cage, ana vidonda, anateseka mnyama wa watu, kwa nini wasimuachie aende kwenye mbuga ili akafe natural death kama wanyama wengine, lakini mnamuweka pale mnampa madawa mnamtunza kuliko binadamu, at the end of the day lazima atakuja kufa tu. Kwa hiyo, wamwache afe kwa kifo chake cha kawaida, lakini siyo mumtunze pale na wakati tunahitaji fedha nyingi kwa ajili ya kutunza hifadhi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, watu wamekuwa wakija sana Northern Circuit, nami niungane na wengine niombe sasa tuweke mkazo Southern Circuit. Southern Circuit kumekuwa ni monopoly, unakuta ni mtu mmoja amejenga hoteli kule, barabara sio nzuri sana kwa hiyo unakuta Wawekezaji wa ndani inawawia vigumu sana kwenda kuwekeza kule kama nilivyozungumza mwanzoni. Licence ni nyingi, fees ni nyingi, unakuta Local Tour Operators ni vigumu sana kwenda kuwekeza kule chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara iweke mazingira wezeshi ili Watanzania nao waweze kwenda kuwekeza kule Southern Circuit, wajenge hoteli tuweze kuuza Southern Circuit, maana yake sasa hivi ukisema unaiuza Southern Circuit huwezi, unakuta ni zaidi ya dola 6,000. Mtu anataka apande mlima, atembee aende Southern Circuit, aende aka-relax Zanzibar, inafika karibu dola 12,000 au 15,000 watu hawawezi ku-afford hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujio wa watalii sasa hivi kuna competition, wenzetu Kenya wanapeleka very cheap kwa sababu ndege zao zinawaleta wageni direct mpaka Nairobi, kwa hiyo inakuwa ni rahisi kwa wao kuweza kuuza utalii Nairobi kwa bei rahisi kuliko ilivyo Tanzania... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kuhusu hali ya usalama nchini. Kwa sasa hivi unaweza kusema kuna utulivu tu; kwa sababu tumeshuhudia siku za hivi karibuni pamekuwepo na matukio mengi sana ya watu kuuawa bila sababu, kwa mfano askari waliouawa huko Kisarawe kwa kupigwa risasa na watu wasiojulikana, matukio kama haya yametokea Pangani na Mwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali imeshafanya uchunguzi wahusika ni akina nani? Watu hawa wanaweza kuanza taratibu uhalifu huu kwa kuanzia pembezoni mpaka wakafika mjini, tutakuwa tumechelewa, je, Serikali inawaeleza nini Watanzania kuhusu matukio haya yanayotishia usalama wa Watanzania?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Jeshi hili linajishughulisha na kazi za maendeleo kupitia vikosi vyake kama ujenzi wa barabara, mpaka gari wamewahi kuunda, na kwa kupitia Jeshi hili tunaweza kuokoa fedha nyingi sana hata kuwapa tender za samani za ofisi za Serikali kama walivyotengeneza madawati, nawapongeza sana. Hata hivyo changamoto kubwa ni utolewaji wa fedha za maendeleo ndiyo unawakwamisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano waliomba shilingi 248,000,000,000/= kwa ajili ya maendeleo lakini wamepata shilingi 35,000,000,000/=, sawa na asilimia 14.5 ya bajeti waliyoomba. Je, kwa ufinyu huu unaotolewa wataweza kutimiza majukumu yao? Hii ni kuwarudisha nyuma, badala ya kuendelea wamebakiwa na kulipa madeni. Tukumbuke Jeshi hili kwa sasa ndilo linalotusaidia kuwajenga vijana wetu kimaadili kwa kwenda jeshini, wale wanaomaliza kidato cha sita. Je mpaka sasa hivi Serikali imeweza kuchukua vijana wangapi kwenda jeshini?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Maji ni uhai, wanadamu, wanyama, mazao kila kitu kinahitaji maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wengi tumekuwa tukilalamikia upatikanaji wa maji katika Jiji letu la Dar es Salaam, tukumbuke Jiji hili ndilo kioo cha nchi yetu, lakini tatizo la maji ni kubwa. Hata baadhi ya maji yanapopatikana siyo salama na safi. Baadhi ya maji yanayotoka yamechanganyika na kinyesi sababu ya miundombinu mibovu na mingine imechakaa, pamoja na Serikali kujitahidi kubadilisha baadhi ya mabomba. Je, ni lini Dar es Salaam watapata maji safi na salama kwa ajili ya kunywa? Tumeshuhudia kipindipindu na magonjwa mengine ya kuhara hayaishi Dar es Salaam sababu inachangiwa zaidi kutokuwa na maji salama na safi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maji taka, bado mfumo wa maji taka ni tatizo Dar es Salaam hata hapa Dodoma. Kipindi cha mvua tumeshudia ndiyo wakati mashimo ya maji taka yanafurika na kusababisha kwanza mji mzima kunuka, kusababisha kulipuka magonjwa na kadhalika. Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua mifumo ya maji taka sababu iliyopo ilikuwa inahudumia watu wachache, kwa sasa Jiji limeongezeka watu wengi zaidi ya milioni nne lakini mfumo ni ule tangu enzi za ukoloni

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Wilaya ya Moshi; pamoja na Wilaya hii kuwepo chini ya Mlima Kilimanjaro lakini bado wananchi wanaotoka kata za Mbokomu, Old Moshi, Kiboriloni, bado kuna tatizo kubwa la upatikanaji wa maji. Mradi wa maji vijijini ulikuwepo lakini maji yake yalitoka na siyo zaidi ya miezi sita. Wanaoteseka ni watoto wa shule badala ya kusoma, wanatumiwa na walimu kwenda kuteka maji na akina mama wanatembea mbali wanabeba maji vichwani, hii ni kurudisha maendeleo nyuma. Je, mpango wa kuleta maji ya uhakika vijijini utakamilika lini badala ya haya maji ya kisiasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu umwagiliaji mpaka sasa wakulima wetu wengi walikuwa wanategemea mvua na hawa wapo zaidi ya asilimia 80. Bado Wizara haijatoa elimu ya kutosha jinsi ya kuvuna maji ya mvua kwa kujenga mabwawa, kujenga mifereji ya kudumu ili waweze kupata maji kwa ajili ya kilimo. Serikali ituletee mikakati na mipango ya kuwawezesha wakulima ili waondokane na kilimo cha kutegemea mvua na kilimo hiki ni cha msimu lini waanze kilimo cha umwagiliaji ambacho kitakuwepo misimu yote? Bila hivyo viwanda tunavyotangaza vya usindikaji vitafanya kazi gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri ya Moshi Mabogini, Wajapani walianzisha kilimo cha umwagiliaji, kilimo cha mpunga walijenga mpaka miundombinu ya maji na kilimo kule kiliendelea vizuri sana, lakini tangu Wajapani waondoke kilimo kile ni kama kimekufa. Wizara imeshachunguza ni kwa nini maji yale yamepungua?

Mheshimiwa Naibu Spika, uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji; miaka ya 1960 na 1970 wananchi walielewa maana ya utunzaji wa vyanzo vya maji. Mfano, Mkoani Kilimanjaro zao la kahawa lilishamiri sana kwa kutegemea umwagiliaji na kutumia mifereji ya asili. Walipanda miti na walivitunza vyanzo vya maji, lakini kwa wakati huu vyanzo vingi vimekauka. Miti inakatwa ovyo, wananchi wanalima pembeni mwa mito na Serikali inaona makosa yote haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wakati muafaka sasa kwa Serikali kurudisha wanafunzi kuwa na vitalu vya miti. Viongozi wa vijiji wahakikishe miti inapandwa na hawalimi kando kando ya mito na kusimamia kwa nguvu zote vyanzo vya maji vifufuliwe.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba nianze na Mamlaka ya Mapato Tanzania. Mimi naomba niwaambie Mamlaka ya Mapato Tanzania ni lazima wawe marafiki wa wafanyabiashara, wao wanaona ni ufahari kwenda kufilisi wafanyabiashara, badala ya kutoa elimu unaenda kufunga akaunti ya mfanyabiashara, unaenda kufunga biashara yake, sasa ukishafunga biashara yake wale wafanyakazi hawatafanya kazi mnakosa pay as earn na mnakosa mapato. Naomba muwaelimishe, hata kama mnawadai wapeni muda walipe hicho mnachokitaka kwa muda lakini na biashara iendelee, mkizifunga zile biashara na ninyi pia mnakuwa mmekosa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la kuhakiki TIN sasa hivi unakuta watu wengi hawaendi kuhakiki TIN zao kwa sababu ukienda kuhakiki TIN unakutana na madeni. Haya yamezungumzwa na wengi, magari yamekaa zaidi ya miaka ishirini, wafanyabiashara unakuta unamdai mtu zaidi milioni 40 lakini mfanyabiashara anapeleka returns kila mwaka, hivi ni kwa nini TRA badala ya kukusanya hayo mapato unamwekea mtu deni mpaka linafika milioni 40 halafu ndiyo unakuja kumpa sasa hivi unamwambia alipe milioni 40.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niungane na wenzangu hii kodi ya road licence ingizwe kwenye mafuta na tozo itozwe kwenye magari ambayo yanatembea barabarani, badala ya ku- frustrate watu, kuna watu kule Moshi wamekufa. Utakuta mtu analetewa deni la milioni 200, kuna Mzee kweli kabisa amefariki pale Moshi hajui atalipaje hizo fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba ndugu zangu mjaribu kuwafanya wafanyabiashara wawe marafiki zetu na Waheshimiwa Wabunge muelewe kwamba hizi pikipiki mlizotoa kwa wapiga kura mna madeni mnadaiwa huko, hakikisheni mnaenda kubadilisha majina na waelimishwe watu wakiuza kifaa chake au ukimkabidhi mtu kifaa cha moto lazima abadilishe jina. Kuna siku 30 za kubadilisha lakini mtu akishauza lile gari hajui kama kuna umuhimu wa kubadilisha jina, badala yake mnakuja kumwaadhibu yule mtu aliyebadilisha jina mnamwambia alipe lile deni nafikiri hii si haki na siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka haraka naomba niulize kuhusu wale waliopanda mbegu DECI, wale walikuwa ni watu waliojikusanya na kesi ilienda Mahakamani na ikaisha. Kuna zaidi ya shilingi bilioni 14 zimelala pale Benki Kuu. Nataka Mheshimiwa Waziri aje atuleze fedha zile zimeenda wapi au ndiyo mtindo wenu wa Serikali mnazitumia bila kuwaeleza, maana yake hapa tulichanga fedha za maafa Arusha tukasikia zinajenga mochuari Mount Meru. Kwa hiyo, hebu tuelezeni zile fedha ziko wako na ni lini mtawapa hawa waliopanda mbegu fedha zao maana yake kuna wengine wameshafariki. Mheshimiwa Waziri akija ku- wind up atuambie ni lini watawalipa hawa waliowekeza fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie EFD machines. Sasa hivi sijui hizi EFD machines zinatumika wapi na wapi. Kwa mfano, Moshi mpaka wamachinga wanatumia EFD machine lakini hapa Dodoma maduka makubwa tu hawatumii EFD machines na mnajua kabisa mlisema wenyewe, Serikali ilisema itazitoa hizi EFD machines bure, hilo zoezi lilianza Dar es Salaam kwenye mikoa mingine ni lini mtatuletea hizo mashine ili wafanyabiashara wadogo wadogo na wao waweze kutumia hizi EFD machine.

Mheshimiwa Menyekiti, EFD machine moja inauzwa shilingi laki nane mfanyabiashara mdogo ni vigumu sana kutumia shilingi laki nane kununua hiyo mashine. Halafu zaidi ya hilo hizi mashine haziko durable zinaharibika haraka sana, ukitengeneza mashine moja si chini ya laki moja mpaka laki moja na nusu. Sasa ni mfanyabiashara gani mdogo ambaye ataenda kununua mashine ambayo inaharibika kila wakati? Ukizingatia umeme wetu ndiyo huo ikiingiza EFD machine kwenye umeme inaweza ikaungua. Unakuta EFD machine zinaharibika kila wakati na inabidi ulipe hela kwa ajili ya kutengeneza hizo mashine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijue utaratibu wenu ukoje. Ni watu gani wanaotakiwa kutumia hizi EFD machines na zinatumika sehemu gani Tanzania, maana yake kuwa Watanzania wanaokaguliwa kila siku na kuna Watanzania wengine wanakaa tu bila kuzitumia. Mheshimiwa Waziri wakati anakuja ku-windup naomba na hilo nalo atuelezee. . (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi ya Ardhi, maelekezo yalitoka kwenye hotuba ya ardhi kwamba wananchi wote wanaomiliki ardhi iwe imepimwa au haijapimwa lazima walipe kodi, sasa ardhi hiyo ambayo haijasajiliwa kisheria italipiwaje kodi? Je akilipia kodi ataweza kutumia receipt hiyo kwa ajili ya dhamana yoyote? Serikali ifuate sheria ndiyo maana tulizitunga ambapo wananchi hulipa kodi kwenye ardhi iliyopimwa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Nyumba (NHC), Shirika hili limekuwa likifanya kazi nzuri kujenga nyumba za biashara na makazi lakini madhumuni ya kuanzisha NHC yalikuwa ni pamoja na kujenga nyumba za bei nafuu ili kila Mtanzania aweze kuishi kwenye nyumba kwa haki. NHC imeshindwa kujenga nyumba kwa bei nafuu kutokana na vifaa vya ujenzi kuwa na bei ya juu sana na kupelekea ujenzi kugharimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuwasaidia wanyonge, lakini kwa mtindo huu wa bei za nyumba wanazoziita ni za bei nafuu za milioni 60 ni mfanyakazi/Mmachinga yupi wa kawaida atakayeweza kulipia bei hiyo? Ushauri, Serikali ishushe kodi kwenye vifaa vya ujenzi kwa nyumba zinazojengwa na NHC ili waweze kuendeleza kazi nzuri wanayojitahidi kuifanya kwa ajili ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba wa vitendea kazi na wataalam, pamekuwepo na uhaba mkubwa wa vitendea kazi na wataalam kwenye kitengo cha kupima ardhi ambako kunapelekea wananchi kwenda kutumia wapima ardhi binafsi na wanatoza pesa nyingi ambapo inapelekea wananchi wengi kutopima ardhi zao. Serikali inapoteza fedha nyingi kwa kutopokea kodi ya ardhi. Je, Serikali imetenga fedha kiasi gani kwa ajili ya vifaa kwa nchi nzima ikiwa ni pamoja na kuajiri wataalam wa kutosha kwa nchi nzima? Mfano pale Moshi Vijijini (Wilaya ya Moshi) hawana vitendea kazi kabisa hata usafiri haupo. Ni kwa nini hata kwa kuanzia wasiwe hata na pikipiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, napenda nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na Watumishi wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya kwa kujaribu kupunguza migogoro ya ardhi. Nawashauri mjaribu kutatua matatizo yaliyobaki kuna uhaba wa wataalam na vifaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mategemeo yangu watachukua maoni ya Upinzani na wayafanyie kazi kwa faida na maendeleo ya nchi yetu na wananchi wetu.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia. Nianze na migogoro ya ardhi katika maeneo ya Hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na malalamiko mengi ya mipaka kati ya hifadhi na wananchi na wafugaji kuingiza mifugo kwenye hifadhi. Hii huchangia maambukizi ya magonjwa kwa wanyama na kusababisha wafugaji na walinzi wa wanyamapori na hifadhi kugombana na wafugaji, kuanza kuua wanyama kama samba na kadhalika. Ni vizuri kabisa katika bajeti ya mwaka huu zikatengwa fedha kwa ajili ya kuweka mipaka katika hifadhi zetu ili kumaliza migogoro iliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la uwindaji wa kitalii. Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii alitangaza kufuta leseni zote za uwindaji wa kitalii, jambo ambalo limeleta mtafaruku mkubwa katika sekta hii. Ijulikane kwamba katika utalii huu mwekezaji anatumia fedha nyingi sana kuandaa miundombinu ya uwindaji; na watalii wa uwindaji wanafanya booking zao hata miaka miwili kabla na wanalipa mapema (advance payment). Sasa leo hii ukikatisha ghafla siyo kuua kabisa utalii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wadau wengi wameshindwa kwenda kufanya maonesho/matangazo yaliyokuwa yafanyike mwakani, lakini mpaka sasa hivi hawana uhakika na biashara zao. Pengine Serikali ina nia njema ya kufanya mnada katika kuuza vitalu vya uwindaji, lakini lazima kufidia wale waliopo; wameshatumia kiasi gani kuendeleza vitalu? Tayari wana booking kiasi gani? Wamekata mingapi kwa miaka mingi? Bila kufanya hivyo, tutapoteza fedha nyingi sana ukizingatia sekta hii huchangia zaidi ya asilimia 17 ya pato la Taifa na huchangia kwa kiasi kikubwa kupata fedha za kigeni. Kwa sasa mapato yameshuka kutoka shilingi milioni 23.58 mwaka 2010 hadi shilingi milioni 11.28 mwaka 2015. Hii ni hatari kwa sekta hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imejaliwa vivutio vingi sana ambavyo vingine havipatikani sehemu nyingine. Mfano, mbuga ya Saadan, bado hazijafanyika juhudi za kutosha kuendeleza kivutio hiki ambacho wanyama wanaenda mpaka baharini. Miundombinu ya barabara siyo mizuri, bado hawajashirikisha sekta binafsi ili waweze kujenga hoteli za kitalii ili kuwavutia watalii wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna haja ya kuiwezesha Bodi ya Utalii ili iweze kutangaza vivutio vyetu, siyo nje ya nchi tu, hata kwa utalii wa ndani bado mwamko ni mdogo kwa wazawa kutembelea mbuga zetu. Nashauri watangaze program ya kutembelea shule na kuwahimiza kutembelea mbuga zetu, yaweza ikawa njia moja ya kupata wazawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado TANAPA haijatangaza Hifadhi ya Mkomazi ipasavyo kwa sababu hii ingeweza kutumika kama day trip kwa watalii wanaokuja kupanda Mlima Kilimanjaro. Wakiwa na siku moja ya ziada wanaweza kutembelea hifadhi hiyo na kuongeza pato la Taifa.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kupata nafasi ya kuchangia mfumo wa utoajia huduma wa afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti kuna haja ya kuimarisha mfumo wa rufaa kuanzia ngazi ya chini kutoka zahanati mpaka ufike hospitali aidha ya mkoa au za kanda. Unakuta wagomjwa wengi wanakimbilia kwenda hospitali za ngazi ya juu sababu zahanati hazina wauguzi wala madaktari, hakuna vitanda vya kupima wagonjwa, hakuna dawa na kadhalika. Wafanyakazi wengi kwenye zahanati ni ward attendant.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuweza kuleta ufanisi kwenye zahanati ni vizuri Serikali ukaangalia upya kule tulikotoka na kurudisha zile shule za kufundishia nurses, assistant clinical officers, midwife, rural medical aid na hawa walikuwa specifically trained kufanya kazi katika ngazi za chini, lakini sasa hawapo. Wangekuwepo na vifaa vikawepo kwa kiasi kikubwa tungepunguza sana vifo vya mama na mtoto ukizingatia wananchi zaidi ya 80% wapo vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali 80% ya bajeti yake ingeielekeza kuimarisha hizi zahanati, watu wengi wangeishia kutibiwa kule na kwa kiasi kikubwa tungepunguza msongamano kwenye Hospitali za Rufaa ambako kwa sasa hivi hata mtu akitaka kutumbuliwa jipu unakuta wanaenda hata Hospitali za Mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri pia kuangalia hii sekta ya kada ya dawa za usingizi. Hawa wapo pungufu sana, kuna haja ya Serikali kuwezesha wengi zaidi waweze kufika mpaka ngazi za chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu nguo za wagonjwa, limekuwa ni jambo la kawaida katika Hospitali za Serikali wagonjwa kutoka na nguo zao majumbani na kulala nazo hospitalini. Hii ni hatari sana kuambukizana magonjwa ya ngozi hata kuleta wadudu kama chawa na kunguni wodini, kila mgonjwa anaotoka mazingira tofauti, ni wakati muafaka sasa kwa Serikali kutenga bajeti kwa ajili ya kununua nguo za wagonjwa wanaolazwa wodini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii huenda sambamba na kuimarisha kitengo cha mapokezi cha emergency. Watu wengi hufia casualty sababu unakuta kitengo hiki sehemu nyingine hazina sehemu ya observation, za kumpumzisha mgonjwa ili ajulikane je, atalazwa au ni mgonjwa wa kupeleka wodini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wagonjwa wengi wenye kuishi na VVU wanapopata magonjwa nyemelezi kama nimonia na kadhalika wanabidi wagonjwa hawa wajinunulie antibiotics wakati wengine hawana uwezo kabisa tu kujua kwamba ni rahisi wao kushambuliwa na magonjwa sababu immune yao ilikuwa imeshuka za ARU ni kwa hii wanapopata magonjwa mengi kupitia kitengo chao cha CTC wasipewe dawa hizo bure?

Mwisho, kwa kuwa kumekuwepo na ongezeko kubwa la magonjwa yasiyoambukiza (NCD) na magonjwa haya yanakumba rika zote ni bora elimu itolewe sasa mashuleni kwa nguvu zote. Wizara ya Afya na Wizara ya Elimu waimarishe elimu ya afya mashuleni.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya siasa nchini si nzuri kabisa. Vyama vingi vilianzishwa kwa Sheria No. 5 ya kuruhusu vyama vingi ndiyo maana hata chaguzi zote zinashirikisha vyama vingi, lakini katika chaguzi za marudio tumeona haki zikivunjwa na upendeleo wa wazi kwa Chama cha CCM. Kwa mfano uchaguzi wa marudio Jimbo la Siha askari polisi walikuwa wanawasindikiza CCM kukusanya maboksi ya kupigia kura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haki haikutendeka, Mawakala wa Vyama vya Upinzani walikuwa wanapigwa na kunyang’anywa karatasi za matokeo mbele ya askari wa Jeshi la Polisi. Hii ilisababisha hata katika Jimbo la Kinondoni baadhi ya raia kupoteza maisha kwa sababu tu ya kutokutenda haki. Hivi kulikuwa na sababu gani zilizosababisha tume kutokutoa barua za mawakala kwa wakati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikutano ya hadhara. Nchi yoyote yenye kufuata sheria na inayoamini katika demokrasia ni lazima ifuate sheria maana Katiba, Ibara ya 18 inaruhusu uhuru wa kuongea na kujieleza lakini ni wazi kabisa wakati huu katika Serikali ya Awamu ya Tano, vyama vya siasa haviruhusiwi kufanya mikutano ya hadhara, hata wananchi wakitoa mawazo yao kwenye mitandao wanashtakiwa na Serikali. Maandamano ambayo ni haki ya kikatiba kupeleka meseji kwa watawala yamekatazwa. Je, Serikali hii inaweza kusema ni nchi yenye kujali haki na demokrasia kwa wananchi wake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Makao Makuu Dodoma. Mpaka sasa juhudi kubwa bado zinahitajika kuuendeleza Mji wa Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi. Bado barabara nyingi hazipitiki. Kwa mfano maeneo ya Kisasa barabara ni mbovu sana. Kuna haja ya kushughulikia suala la majitaka, system iliyopo ilikuwa inahudumia watu wachache, sasa hivi idadi imeongezeka, la sivyo yaliyokuwa yanatokea Dar es Salaam kwa maji machafu kufurika ovyo barabarani yatatokea hapa Dodoma na kusababisha magonjwa ya mlipuko kama kuhara, typhoid na kipindipindu kutokea hapa. Je, Serikali ina mikakati gani ya kuongeza njia za majitaka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sambamba na kuongeza shughuli za kijamii kuufanya Mji wa Dodoma kuwa kati ya miji ya vivutio kwa watalii. Kuna vivutio kama mashamba ya zabibu na miamba na mawe; mji utengenezwe uvutie watalii, hata Bunge lenyewe ni kivutio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kilomo. Wananchi zaidi ya asilimia 80 ni wakulima na wengi sana walihamasika kulima mahindi, lakini zao hili limekuwa ni mwiba kwa wakulima. Kama tujuavyo mbegu za mahindi ya kisasa huwa zinaharibika haraka sana na storage yake ni ghali sana na wakulima wengi hawawezi nunua matenki ya kuhifadhi. Bei ya mahindi imeshuka sana inapelekea mahindi kupekechwa na wakulima kupata hasara. Je, Serikali ina mikakati gani ya kuwasaidia wakulima hawa kupata masoko ya kuuza hata nje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzo, mfano Kilimanjaro, ilikuwa haina shida kuuza mahindi Kenya, lakini sasa mpaka upate kibali na vibali vyenyewe kuvipata ni shida na imejaa urasimu mkubwa. Je, Serikali hainunui tena mahindi kwa ajili ya Ghala la Taifa
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Viwanja vya Michezo. Mkoa wa Kilimanjaro kila mwaka wiki ya kwanza ya mwezi wa tatu panakuwepo na mbio za Kilimanjaro Marathon. Mbio hizi kwa sasa zimezidi kukua mwaka hadi mwaka na zinahusisha wageni kutoka nje ya nchi na wenyeji Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbio hizi zinachangia sana uchumi kwa wakazi wa Moshi na Taifa kwa ujumla kwa sababu wageni zaidi ya kukimbia pia hufanya utalii wa kupanda mlima na kutembelea mbuga zetu za wanyama. Mbio hizi kwa sasa kuanzia uwanja wa Chuo cha Ushirika Moshi na kumalizikia pale. Hata hivyo, kwa jinsi mbio hizi zilivyopata umaarufu uwanja ule unalemewa na wingi wa watu ambao ni hatari kwa maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Moshi tuna uwanja mkubwa wenye michezo zaidi ya saba unaoitwa King Memorial Stadium, lakini uwanja huu hautumiki ipasavyo ukizingatia kuwa hakuna viwanja vya michezo Moshi na huu uwanja unamilikiwa na mkoa. Kwa sasa ni sehemu ndogo tu inayotumiwa na wauza nguo za mitumba. Je, ni kwa nini Serikali isitafute watu binafsi kwa kushirikiana na Serikali wakakijenga kile kiwanja ili kiweze kutumika hata kwa michezo mingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa kuwa kilipewa jina la mfalme wa Uingereza naamini likiandikwa andiko zuri mfalme anaweza kukijenga kiwanja kile na tukaendelea kukiita King Memorial Stadium. Hii itachangia Serikali kupata

mapato yatokanayo na uwanja huu, itatengeneza ajira na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utamaduni; hivi utamaduni wa Mtanzania ni upi? Ni siku nyingi tumekuwa tukilizungumzia Vazi la Taifa na kuna wakati ilitolewa mifano ya Vazi la Taifa lakini hadi leo hatujaelezwa mchakato ule ulifikia wapi. Ni lini tutapata Vazi la Taifa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, misingi ya utamaduni wetu Watanzania ulijengwa tuwe na utu, upendo, amani na utulivu lakini kwa sasa nchi yetu tunaelekea kupoteza vyote hivi na mpaka sasa hivi Serikali haijaweza kutueleza hao watu wasiojulikana ni akina nani? Watu wamekuwa wanatekwa, wanauawa na kuokotwa baharini kwenye viroba, waandishi wa habari wanatekwa, yote haya ni amani, upendo, utu na utulivu kutoweka. Je, Serikali inatueleza nini kuhusu utamaduni wetu huu kupotea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Haki ya Kupata Habari. Hii ni haki ya msingi ambayo ipo kikatiba kabisa ya watu kupata habari; lakini tumeshuhudia sasa hivi Serikali imekuwa ikivifungia vyombo vya habari pindi wanapoikosoa Serikali. Pia ni haki ya Watanzania kuona wawakilishi wao Bungeni kama wanazizungumzia kero zao, lakini haki hii wamenyimwa kwa kuzuiwa kwa Luninga (TV) kutokuwa mubashara (Live) wakati vipindi vya Bunge vikiendelea. Huu ni uvunjwaji wa sheria, inapelekea nchi kuendeshwa bila kufuata sheria.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kwanza kwa kuwa mchangiaji wa kwanza katika Wizara hii ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda Serikali itueleze ni kwa kiasi gani wanajiandaa kuweza kutenga ile asilimia 15 ya bajeti ili waweze kutekeleza lile Azimio la Abuja? Wasipofanya hivi wanashindwa kutekeleza mambo yao ya maendeleo, wanashindwa kujenga vituo vya afya na kupata vifaa kwa ajili ya hizi hospitali. (Makofi)



Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie KCMC. Napenda niwapongeze sana KCMC, Mheshimiwa Waziri ameeleza kwamba wametibu wagonjwa 1,100 wenye matatizo ya saratani na wanaweza wakafanya vizuri zaidi. Wamejaribu kutafuta wafadhili, wamewafadhili wamepata vifaa vyote vya mionzi na kila kitu wamepata kwa ajili ya ile unit ya saratani. Kinachopungua pale ni lile jengo banker kwa ajili ya mionzi. Wanahitaji karibu shilingi bilioni tano, lakini mnaweza mkawasaidia kwa kuwapa kwa awamu. Siyo lazima muwape yote kwa pamoja. Mkiweza kuwapa hizo fedha kwa ajili ya kujenga ile banker itawasaidia sana kupunguza msongamano katika Hospitali ya Ocean Road.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba yake nimeona Mheshimiwa Waziri anatoa sana fedha nyingi kwa ajili ya Ocean Road, lakini pia KCMC ikisaidiwa, mtasaidia sana hii Kanda ya Kaskazini kupunguza msongamano katika Hospitali ya Ocean Road. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niizungumzie hospitali yetu ya Mkoa wa Kilimanjaro ambayo ni Hospitali ya Mawenzi. Hospitali ile Mheshimiwa Waziri naomba itupiwe jicho. Ni Hospitali ya Rufaa lakini haina Emergency Unit. Tunaomba mhakikishe kuna Emergency Unit na iwe fully equipped, kuwe na timu ambayo inaweza ikahudumia wakati wa emergency.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Hospitali ya Mawenzi haina isolation room. Unakuta mgonjwa ana TB analazwa na mgonjwa mwenye malaria. Sasa mgonjwa mwenye malaria anaenda hospitali kutibiwa malaria akirudi nyumbani anaweza akapata TB. Kwa hiyo, tunaomba sana mtuhakikishie kwamba kunakuwa na isolation room pale Mawenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kile Kitengo cha Wagonjwa wenye Matatizo ya Akili kwa kweli kiko kwenye hali mbaya sana. Wale wauguzi wanafanya kazi pale lakini unakuta saa nyingine hawa watu wenye magonjwa ya akili wanaweza wakawapiga. Sasa kutoka kule kwenye wodi ya wagonjwa



wenye akili mpaka waweze kupata msaada, hamna hata kengele ya kuweza kupiga ili waweze kusaidiwa. Kwa hiyo, unakuta wale wauguzi wana shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo kuna ile rehab ambayo ina-serve kanda nzima ya Kaskazini, lakini ile rehab imesahaulika kabisa, haina uzio, hawapewi hata sabuni, hawapewi vyakula, unakuta watu wanajitolea kusaidia. Sasa nataka kujua hii Serikali mnasema mnawasaidia wanyonge, hapa mnawasaidia wanyonge kweli? Kwa sababu wale wanaoenda kule unakuta wengine hawana hata familia, wamekaa tu pale wameachwa hamna dawa. Ukiangalia madaktari, hawapo wa kutosha. Sasa sijui mna mpango gani wa kuhakikisha kwamba tunapata madaktari wa kutosha katika kada hii ya wagonjwa wenye matatizo ya akili? Kwa sababu nasikia ni madaktari 26 tu nchi nzima tulionao. Sasa kwa mtindo huu, sijui ni kwa jinsi gani mtaweza kuwasaidia hao wanyonge ambao mnasema mnawasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna upungufu mkubwa wa Madaktari wa Nusu Kaputi. Sijasikia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ni kwa kiasi gani mnaenda ku-train hawa madaktari wa nusu kaputi. Napenda Mheshimiwa Waziri wakati anakuja ku-wind up atuelezee ni nini anachoenda kufanya ili tuweze kupata madaktari wa kutosha wa nusu kaputi.

Sasa hivi tumeona kuna mafuriko yametokea katika Mji wetu wa Dar es Salaam na Morogoro. Tunajua mafuriko yakitokea kutakuwa na magonjwa ya mlipuko. Dar es Salaam mafuriko yakitokea watu ndio wanafungua yale ma-septic tank, kwa hiyo, unakuta maji yanachanganyika na vinyesi na tunajua kipindupindu kwa lugha ya sisi ambao sio Madaktari ni kwamba mtu amekula kinyesi. Sasa sijui Serikali mna mpango gani au mmejitayarishaje kuhakikisha kwamba magonjwa ya milipuko yakitokea mnaenda kui-handle namna gani? Kwa sababu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna tatizo kubwa la wanafunzi kuwa na uwezo wa kusoma, kuhesabu hata kuandika katika shule zetu za msingi za Serikali. Hii inatokana na ripoti ya dunia ya 2014. Watu wengi wanakosa ujuzi wa mbinu za elimu za kufundishia. Hii inachangia pia na watu wengi kutokupata motisha kazini, hawalipwi madai yao; sehemu kama vijijini unakuta hakuna nyumba za walimu za kuishi, shule nyingine hazina madarasa, baadhi ya wanafunzi huketi chini, hakuna vitabu, baadhi ya shule unakutana na walimu wawili tu na ndio wanafundisha masomo yote kuanzia darasa la awali mpaka darasa la saba. Je, kwa vitendo hivi patakuwepo na ufaulu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha idadi ya walimu wa shule za msingi imeshuka kutoka walimu 191,772 mwaka 2016 hadi kufika 179,291 mwaka 2017. Hili ni anguko la 6.5% na kupelekea mwalimu mmoja kufundisha kwa uwiano wa 1:50 ukizingatia uwiano unaokubalika ni mwalimu 1:25.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuwa na nyumba imara lazima msingi uwe imara. Hii inapelekea mpaka kuelekea sekondari, wanafunzi hawafanyi vizuri sababu ya upungufu wa walimu wa hisabati 7,291, baiolojia upungufu 5,181, kama upungufu 5,373; na fizikia 6,873. Takwimu hizi zinatokana na BEST 2016.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika karne hii ya sayansi na teknolojia hapa Tanzania Serikali itakuwa inatafuta wataalam kutoka nchi za nje. Sioni ni kwa jinsi gani tunaweza kuzalisha wanasayansi wetu kwa mtindo huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ina mikakati gani wa kushughulikia tatizo la upungufu wa walimu wa shule za msingi na sekondari? Kwa mwaka 2018 Serikali imejipanga kuajiri walimu wangapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana kuwekeza katika elimu, lakini bajeti imekuwa ikiidhinishiwa bajeti pungufu, mfano mwaka 2017/2018 Bunge iliidhinisha shilingi bilioni 4.7064 kwa sekta ya elimu, lakini ilipungua kwa 1.3% ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2016/2017 ambayo ilikuwa ni shilingi bilioni 4.7707 nayo ilipungua kwa shilingi bilioni 64.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado Serikali inashindwa kutenga 20% ya bajeti kwa ajili ya sekta ya elimu na kupelekea Wizara kushindwa kutimiza majukumu yake. Kwa mwelekeo huu, ubora wa elimu hapa nchini hauwezi kupanda hata kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo ni jukumu la Serikali kuhakikisha inatenga fedha za kutosha ili waweze kutenga fedha za kumsaidia mtoto wa kike aweze kuhudhuria shuleni kwa siku zote, kuhakikisha vyoo vyote vinakuwepo na maji na kuwekeza katika utoaji wa taulo za kike bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni lini walimu watalipwa posho na madai yao yote ukizingatia wengine wapo katika mazingira magumu sana ya kazi, wengine wana mikopo na kadhalika?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala la ukarabati wa zahanati na vituo vya afya. Ni jambo zuri la Serikali kujenga zahanati kila kijiji na vituo vya afya kila kata. Lakini vipo vituo vilivyopo ambavyo ni chakavu na havina wahudumu wa afya na vifaa. Ushauri, Serikali ingeviimarisha vile vilivyopo kwanza na kuhakikisha kuna vifaa, madaktari na manesi na dawa na hii kwa kiasi kikubwa itapunguza sana msongamano kwenye ngazi za juu Wilaya hadi Mkoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu magonjwa yasiyoambukiza (NCD), pamekuwa na ongezeko kubwa sana la magonjwa yasiyoambukiza kama ugonjwa wa sukari ya kupanda na kushuka, shinikizo la damu ya kupanda na kushuka, magonjwa ya moyo na kadhalika. Magonjwa haya mengi yanachangiwa zaidi na mtindo wa maisha, vyakula tunavyokula na kutofanya mazoezi ya mwili. Inasemekana karibu asilimia 10 ya wananchi wana uzito uliopitiliza (obesity).

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri, elimu itolewe zaidi na Wizara ishirikiane na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ili barabara zinapojengwa wahakikishe wanajenga pavement ya wapita kwa miguu au kuendesha baiskeli, hili ni zoezi zuri sana. Wafanyakazi badala ya kwenda na magari kazini wanaweza kutembea na pia ofisi zote zinaweza kuwa na chumba cha kufanyia mazoezi kwa kufanyia mazoezi; kwa kufanya hivi Serikali itaokoa kwa kiasi kikubwa fedha kwa ajili ya matibabu. Pia pawepo na vipimo vya kupima sukari na shinikizo la damu kwenye maofisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ugonjwa hauna muda, mama mjamzito akija kujifungua anaweza pata uchungu muda wowote. Sehemu za vijijini wanawake wengi wanapoteza maisha kutokana na umbali wa kufika hospitali ya ngazi za juu. Je, kwa nini zahanati zisifanye kazi kwa muda unaozidi masaa nane? Sababu hizi ndizo zilizopo karibu na wananchi au pawepo na gari (ambulance) masaa 24 itakayosaidia kuwakimbiza wagonjwa kwenye kituo cha afya au ngazi ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upandikizaji wa figo; napenda kuipongeza Serikali kwa jitihada hizi kubwa na kuweza kuwasaidia watu wengi waweze kupata huduma hii ambayo ni ghali sana. Swali langu ni kwmaba kwa kuwa mtu akishapandikizwa figo ni lazima atumie dawa kwa maisha yake yote na dawa hizo ni ghali sana, je, Serikali imejipangaje kuhakikisha wagonjwa hawa watazipata dawa hizo kwa sababu sio kila mgonjwa atakuwa na uwezo wa kununua dawa hizo?

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona wagonjwa wengi wanaomba msaada wa matibabu kupitia magazeti, televisheni na wengine wamepewa barua kutoka Ofisi za Serikali kutoka kwa Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mkoa kuwaombea misaada ya matibabu, je, ni jukumu la Serikali kuruhusu wagonjwa hawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tatizo la vifo vya akina mama vitokanavyo na uzazi ni kubwa sana hapa nchini na badala ya kupungua vinaongezeka. Kuna haja ya kuliangalia suala hili kwa umuhimu sana na kuhakikisha vifaa na wakunga wanakuwepo wa kutosha; na upungufu wa wataalam naamini unachangia vifo hivi.

Mwisho kabisa niwapongeze Waziri na Naibu Mawaziri wanavyojitahidi katika sekta hii, lakini tukumbuke wote sisi ni wazee wa kesho, kambi za wazee mfano iliyopo Moshi Manispaa (Njoro) ipo katika hali mbaya, malazi sio mazuri hata vyoo vyao sio vizuri. Naomba Serikali iende ikakague kituo hicho ili waweze kuwasaidia wazee.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai na ni rasilimali muhimu sana kwa maendeleo ya binadamu katika kila sekta, kilimo kinahitaji maji, viwanda, binadamu, wanyama na viumbe vyote hai bila maji haviwezi kuishi, hivyo maji ni kitu muhimu sana kwa uhai hata mwisho wa uhai wa mwanadamu bado hawezi kuzikwa lazima atumie maji kusafishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji safi na salama bado ni tatizo katika Mikoa mingi mfano hapa Dodoma bado maji siyo salama kupelekea wananchi wengi kupata magonjwa ya mlipuko na pia kuwepo na typhoid. Kwa kuwa Dodoma ni Makao Makuu na ni mji tunategemea kuwepo na ongezeko kubwa sana la watu. Je, Serikali ina mkakati gani ya kuboresha mfumo wa maji taka kuwa mkubwa zaidi ili uweze kubeba maji yote na kuwepo na dampo la kutupa taka? Hii ikiwa ni sambamba na kupata maji safi na salama ya kunywa. Kwa mfano, Manispaa ya Moshi mbona ina maji safi na salama kama iliwezekana kule, hata hapa itawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mradi wa maji uliopo Jimbo la Moshi Vijijini, Kata ya Mbokomu mradi uliofadhiliwa na ADB, mradi huu umejengwa chini ya kiwango na chanzo cha maji kilivyojengwa hakina uwezo wa kudhibiti uchafuzi wa maji isitoshe maji yameelekezwa kwenye chamber ya bomba kwa kutumia mfumo ya sandarusi (sulphate) iliyojazwa udongo na chamber ya kutolea maji ilifunikwa bati yenye kutoa kutu hivyo maji kupita kwenye bomba bila kuchujwa, hii ni hatari sana kwa afya za wananchi wa kule. Nashauri Serikali ije itembelee mradi ule uliojaa ufisadi, isitoshe hata maji ya uhakika hayatoki na ichunguze walioidhinisha kwa kutia saini kwamba mradi huu wa maji umekamilika na kuidanganya Serikali ili wawajibishwe na mradi ule ule ukarabatiwe upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la kutua mama kubeba maji kichwani hasa vijiji bado ni tatizo kubwa sana la maji, Serikali imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya maji vijijini na miundombinu yake lakini panakuwepo na changamoto nyingi mfano kufikia mwaka 2018 Serikali kwa kushirikiana na wadau ilijenga vituo mbalimbali 125,068; vituo hivi vilikuwa vihudumie watu milioni 30.9 sawa na asilimia 85.2 ya wananchi milioni 36.3 wanaoishi vijijini, cha kusikitisha ni vituo 86,877 pekee vinavyotoa huduma kwa watu milioni 21.7 sawa na asilimia 59.8 ya wananchi waishio vijijini. Hivyo vituo 38,209 vilivyojengwa havifanyi kazi sawa na asimilia 30.5 ya vituo vyote. Je, kwa mtindo huu Serikali ina mikakati ya ukweli ya kumtua mama kubeba maji kichwani?

Mheshimiwa Naibu Spika, je, mpaka sasa Mfuko wa Maji una kiasi gani, Serikali ina mpango gani? Bado naendelea kutoa pendekezo la kutoza shilingi 50 kwenye mafuta ili zirudi kwenye Mfuko wa Maji. Ni lini mradi wa maji uliopo Kata ya Old Moshi Magharibi, Jimbo la Moshi Vijijini, kijiji cha Manda utakamilika?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Waziri mara nyingi nimekuwa nikizungumza naye kuhusu kilio changu cha barabara ya Old Moshi - Kiboroloni - Kikarara - Tsuduni. Mheshimiwa Waziri anafahamu kabisa umuhimu wa barabara ile, ni barabara ambayo KINAPA ime-identify kama njia ya kupanda mlima kwa ajili ya watu mashuhuri, lakini kwa sasa hivi barabara ile haipitiki, ni mbaya, lakini mmekuwa mkitupa matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016/2017 kwenye kitabu cha Waziri alitenga shilingi bilioni 2.583; kwa mwaka 2017/2018 mkatenga shilingi milioni 811 na mwaka 2018/2019 ukurasa wa 198 mmetenga shilingi bilioni moja. Naomba commitment ya Mheshimiwa Waziri, TANROADS Makao Makuu wamesema wameshauza tender na upembuzi yakinifu unaendelea, ni lini sasa barabara ile itaanza kutengenezwa badala ya kutuwekea tu fedha kwenye makabrasha lakini hamtengi fedha hizi. Naomba atueleze ni lini sasa barabara ile itaanza ili wananchi wa kule Old Moshi waweze kufaidika ili na Serikali iweze kupata mapato kutokana na ile njia ya kupanda Mlima Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sio hilo tu lakini Moshi Airport imesahaulika kabisa. Mlisema mnatenga fedha kwa ajili ya Moshi Airport, uwanja huu ni very strategic. Wageni wakija kupanda Mlima Kilimanjaro wanaweza wakatumia Moshi Airport wakaruka wakaenda Seronera ambayo ina- save time na wakaweza kwenda mpaka Zanzibar, lakini uwanja ule sasa hivi umekuwa ni wa kulima maharage na karanga. Sasa sijui Mheshimiwa Waziri ana mpango gani maana tayari airport iko inaweza ikatumika pia kwa emergency landing. Atakapokuja ku-windup atatueleza wana mikakati gani kwa ajili ya Moshi Airport. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongee kuhusu reli ya Dar es Salaam mpaka Arusha; sijaona katika mkakati wana mpango gani na reli ile. Tumekuwa tunalalamika barabara zetu zinaharabika, malori yanabeba mizigo mizito sana inaharibu barabara, lakini ile reli ingeweza kutumika ikabeba mizigo ikapeleka Arusha, mizigo ingetoka Tanga ambako kuna bandari ikaletwa Dar es Salaam au Moshi kwa njia ya reli. Sasa hivi tunatumia malori halafu barabara zinaharibika na tunalalamika malori yana-overload lazima ya-overload kwa sababu wanahitaji fedha, lakini tungetumia treni na kukawa na treni ya wageni pia wageni wangeweza kutumia kama scenery kwa ajili ya kuangalia nchi yetu na vivutio vyetu kupitia reli.

Mheshimiwa Naibu Spika, TAMESA ilijengwa mikoa yote ili kuokoa fedha za Serikali za kutengenezea magari ya Serikali. Tayari TAMESA kuna mashine na vipuri kwa ajili ya kutengeneza magari, lakini vimepitwa na wakati, miundombinu iko pale lakini kwa nini hawatengi fedha ili waweze kununua miundombinu ya kisasa ili gari za Serikali ziweze kwenda kufanyiwa service kule TAMESA ili kuokoa fedha za Serikali? Sasa hivi TAMESA wamekuwa ni wakala wa private sector badala ya TAMESA kutengeneza magari wamekuwa wakitoa barua wanawapa Serikali, Serikali inaenda kupeleka kwa Mchina wanaenda kutengeneza gari hizo, sasa huu siyo ufisadi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atueleze ni kwa jinsi gani wamejiandaa kuirudisha TAMESA iweze kufanya kazi ili tuweze kuokoa fedha nyingi ambazo zinapotea kwenye private sector. Maana yake hamuwalipi kwa wakati wanaongeza 10% au pengine hawa watu wa Serikali ndiyo wanaoongeza 10% unakuta matumizi ya Serikali yanakuwa makubwa sana. Hamuwalipi wakati na wao wenyewe wamekopa benki mwisho wa siku unakuta fedha zinakuwa ni nyingi sana kwa wale ambao wanatengeneza magari TAMESA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, naomba niungane na wenzangu kuzungumzia TBA. Nyumba za TBA ni mbaya na mbovu. Sasa hivi TBA wamepewa zile nyumba za Uhindini, zilizokuwa za CDA, huwezi kuamini mtu anaweza kuishi pale. Mmewahamisha wafanyakazi kutoka Dar es Salaam mnakuja kuwaweka kwenye yale magofu, hivi huu ni utu? Mtu kaacha nyumba yake Dar es Salaam, familia yake, watoto wake mnakuja kuwaweka kwenye haya magofu?

Mimi nataka kujua Serikali mtaiwezeshaje TBA ili waweze kutengeneza zile nyumba watu waweze kuingia ndani waishi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kiisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa Serikali itueleze viwanda vilivyobinafsishwa mwaka1992, kati ya156 ni vingapi vinavyofanya kazi na visivyofanya kazi ni vingapi na wale waliopelekea hasara hii wamechukuliwa hatua gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi walio wengi zaidi ya asilimia 80 wanaishi vijijini na kule ndiko kilio kilipo, pamoja na Serikali kupeleka umeme vijijini lakini umeme ule ni mdogo sana hata kuwasha taa. Serikali iliahidi kuwekeza katika viwanda vidogo vidogo lakini vimeshindwa kabisa, lazima pawepo na mgongano wa biashara,vyakula viwe process kule kule vijijini na hii itasaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana kutokimbilia mjini kutafuta ajira na wengine kuingia katika vitendo viovu. Serikali ije na itueleze nia na mikakati gani ya kuhakikisha mazao yanaongezewa thamani kule kule ili wakulima wapate faida. Hivyo lazima pawepo na viwanda vidogo na vya kati huko vijijini. Wakulima wengi sasa hivi mazao yao yanaozea kwenye maghala kwa kukosa masoko, mfano mahindi na mbaazi wakulima wengi sana wamepoteza mitaji hata ya kuendeleza kilimo chao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mji wa Moshi ulijulikana sana kwa kuwa na viwanda vya misumari, ngozi, makaratasi, viberiti mpaka kiwanda cha dawa lakini sasa hivi kinachofanya kazi tena kwa kuharibu mazingira ya Moshi, harufu mbaya inayochangia afya ya wakazi wa Pasua na Boma Mbuzi ni Kiwanda cha Ngozi. Je, Serikali ina mikakati gani hata ya kufufua Kibo Match, viwanda hivi vilichangia sana kupata ajira kwa vijana wetu lakini cha kusikitisha kwa sasa vingi vimeugezwa kuwa stoo za kuhifadhia vitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda bila kuwa na umeme na maji ya uhakika tutakuwa tunaviongelea viwanda hivi kwenye vitabu na cha zaidi mazingira ya kufanya biashara hapa nchini ni magumu sana, mpaka mfanyabiashara apate kibali cha kufanyia biashara inaweza hata kutumia zaidi ya mwezi. Pia mfumo wa kodi na tozo ni nyingi mno na hii inachangia wafanyabiashara wengi kufanya biashara au kuhama na kwenda kuwekeza kwenye nchi nyingine. Serikali ifanye kazi kwa pamoja kabla TRA haijatoa makisio, basi wawapatie leseni wafanyabiashara wafanye kazi nchini wajue wanawapa makisio ya kiasi gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei za bidhaa zimekuwa hazipo elekezi Serikali inatoa tu matamko ya kisiasa mfano ilitoa tamko sukari iuzwe shilingi 2,500 kwa kilo lakini sukari inauzwa mpaka shilingi 3,000 kwa kilo sababu hakuna chombo kinachofuatilia bei hizi. Hivi Tume ya Bei (Price Commission) haipo? Pamoja na masoko kuwa huria lakini lazima Serikali iangalie ni jinsi gani wataweka system ya kufuatilia bei za bidhaa kwa wananchi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitafuta mwekezaji kwa ajili ya kiwanda mama cha Machine Tools kilichopo Kilimanjaro. Pamoja na vipuri kupitwa na wakati lakini majengo bado yapo, sasa Serikali imefikia wapi kupata uwekezaji wa kuendeleza kiwanda hiki ambacho kingekuwa mkombozi wa kutengeneza viwanda vidogo na vya kati ili viweze kufanya kazi vijijini?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Naibu Spika, barabara iliyopo Mkoa wa Kilimanjaro Wilaya ya Moshi, Kata ya Old Moshi Mashariki kuanzia Kiboriloni – Kikarara – Tsudini mpaka Lango la Mlima Kilimanjaro, barabara hii ilikuwa ahadi ya Mheshimiwa Rais Mstaafu, Dkt. Jakaya Kikwete na baadae kupewa ahadi na Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli. Ni zaidi ya miaka 10 imekuwa ikitengewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa lami lakini mpaka leo inafanyiwa upembuzi yakinifu. Je, zoezi hili linachukua muda gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ile kwa umuhimu wake kwenye sekta ya utalii ambayo Wizara ya Maliasili inaifanya njia ya Old Moshi kwa ajili ya watu mashuhuri lakini cha kusikitisha barabara ile imeharibika sana, haipitiki kabisa. Kinachoonekana kule ni vibao vya TANROADS vinavyoashiria wataanza kutengeneza lakini hakuna kinachoendelea!

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inahamia Dodoma rasmi lakini bado kuna Wizara pamoja baadhi ya barabara zipo TARURA sababu hapa ndiyo kioo cha nchi yetu ni lazima tuanze kuwa na mipango ya kuhakikisha barabara zote zinapitika kwa lami na kuwepo na njia za ring roads ili kuzuia msongamano, la sivyo, kile kichefuchefu cha foleni ya Dar es Salaam kitahamia Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja wa ndege uliopo Moshi umesahaulika kabisa, kwa sasa uwanja ule wananchi wanautumia kwa ajili ya kilimo cha maharage. Uwanja ule upo very strategic kwa ajili ya kukuza utalii, unaweza kutumika kwa dharura, pia kutumika kwa ajili ya ndege ndogo kupeleka watalii Serengeti National Park baada ya kupanda mlima. Je, Serikali ina mikakati gani ya kukikarabati au kukifufua kiwanja cha ndege cha Moshi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu karakana iliyopo Kilimanjaro International Airport, karakana hii ipo pale KIA lakini haitumiki ipasavyo, ingeweza kuchangia kwa kiasi kikubwa kuongeza fedha za kigeni. Ndege kutoka nchi jirani zingeweza kuja pale na kufanya service, kupiga rangi na kadhalika, lakini Serikali haioneshi nia ya dhati ya kukarabati karakana ile. Je, ni lini Serikali itaanza ukarabati katika karakana ya KIA ili iweze kuchangia katika Pato la Taifa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu TAMESA, nia ya kujenga TAMESA kila Mkoa ilikuwa ni njia mojawapo ya kupunguza matumizi kwenye magari ya Serikali na magari yote ya Serikali yatengenezewe kule na kufanyiwa service kule, lakini karakana hizo vipuri vyake vimepitwa na wakati na magari yaliyopo sasa ni automatic na teknolojia mpya, badala yake TAMESA inatumika kuegesha magari ya Serikali yasiyofanya kazi kabisa na kwa sasa gari ya Serikali inapelekwa TAMESA halafu TAMESA wanawapa kibali kwenda kutengeneza au kufanya service kwenye garages za watu binafsi. Hii inasababisha Serikali kuwa na madeni makubwa sababu kule private malipo huwa zaidi ya hata mara mbili na sababu ni kwamba pia Serikali inachukua muda mrefu kuwalipa madai yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kujua Serikali ina mikakati au mipango gani ya kuhakikisha inaweka teknolojia ya kisasa katika karakana zote sababu miundombinu ipo ili magari ya Serikali sasa yaanze kutengenezewa TAMESA hatimaye kupunguza gharama kwa Serikali?

Mheshimiwa Naibu Spika, nyumba nyingi za TBA zipo katika hali mbaya sana, mfano hapa Dodoma, nyumba zilizokuwa chini ya CDA ni mbovu kupita kiasi na Serikali imewapangia wafanyakazi wanaohamia hapa kuishi kule. Naiomba Serikali itambue wafanyakazi hawa walitoka majumbani kwao, nyumba zenye hadhi leo hii TBA mnawapangia nyumba ambazo bado hamjazikarabati kabisa? Majengo mengi yamefubaa hakuna sababu ya kuyabomoa lakini wakarabati ili kuwepo na kumbukumbu ya majengo hayo kwa vizazi vijavyo kujua Dodoma kabla ya Makao Makuu kuhamia Dodoma ilikuaje. Historia ni muhimu sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nnianze na masoko ya mazao. Kama tunavyojua wananchi zaidi ya asilimia 80 wanaishi vijijini na kule ndipo wakulima wa mazao tofauti walipo. Kwa mfano mkulima wa mahindi anajitahidi analima, palizi, vibarua, dawa na kuvuna kwa kutumia fedha zake. Lakini Serikali inaweka bei elekezi ya kuuza mahindi na kwa sasa hivi bei ya mahindi imeshuka hadi shilingi 30,000 kwa gunia, isitoshe kama tujuavyo mahindi ya kisasa huwezi kuhifadhi bila dawa na ukitaka kuhifadhi bila dawa ni kutumia ma-tank ambayo ni ghali sana kuanzia magunia 100 tani ni shilingi milioni tatu mpaka shilingi milioni 2.8; sasa kwa kukatishwa tamaa huku mkulima anaweza kununua hiyo storage?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamekuwepo na mazao kama nyanya na matunda mbalimbali, kwa nini Serikali (Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda) visiwawezeshe wakulima kupata viwanda vidogo vidogo vya kusindika mazao kule kule vijijini halafu wanavipeleke kwenye viwanda vya kati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo Gairo kuna wakulima wengi sana wa nyanya wangeweza kusindika na nyanya na kupeleka kwenye Kiwanda cha Tomato Sauce kilichopo Iringa cha DABAGA, pia kuna kiwanda kinachoitwa DASH kipo Iringa lakini hakina malighafi ya kutosha na hii pia baadhi ya nyanya hazikidhi viwango, kuna haja ya wataalam (Maafisa Ugani) waende wakatoe elimu kwa wakulima na kuwashauri kuhusu mbegu bora na dawa zipi za kutumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha ndizi ni kati ya zao kubwa sana linalokubali katika mikoa ya Kilimanjaro, Kagera, Mbeya, Morogoro na kadhalika, lakini zao hili Serikali halijalichukulia kama zao linaloweza kutuingizia fedha za kigeni. Zao hili la ndizi kwa nchi kama Uganda wamekuwa waki-export kwenda nchi za Ulaya na zinauzwa kwa bei ya juu sana peace tano tu za ndizi ni sawa na pound za Uingereza tatu sawa na shilingi 9,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri sasa Serikali kutoa elimu pia jinsi ya ku-pack ili tuweze ku-export zao hili. Tukitumia Balozi zetu kwenye Kitengo cha Biashara watafute masoko kule ndio kazi yao. Hili liende sambamba na matunda kama parachichi, maembe na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba wa pembejeo na ukosefu wa mbegu bora hili limekuwa ni tatizo sasa. Kila hotuba ya bajeti tumekuwa tukiulizia suala hili na yote haya yanasababishwa kwa nchi kushindwa kuzalisha mbegu na viwanda vya pembejeo. Ushauri tunaweza kushirikisha jeshi, wafungwa kwa kutumia wataalam tukazalisha mbegu zetu na zenye ubora, Serikali iwajali wakulima.
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru. Utalii unachangia asilimia 17.5 kwenye Pato la Taifa, lakini utalii ungeweza kuchangia zaidi kama tungeweza kuwekeza katika kuiwezesha TTB iweze kutangaza utalii zaidi.

Mheshimiwa Spika, ni jambo la kusikitisha TTB inapewa 2.4 billion kwa ajili ya matangazo, watatangaza nini? Kutangaza CNN tangazo moja tu ni shilingi bilioni 1.2, wakienda kwenye maonesho/exhibition, mfano wameenda Ujerumani ITD, pavilion moja ni zaidi ya shilingi milioni mia nne, sasa watatangazaje utalii wa Tanzania?

Mheshimiwa Spika, uki-compare na nchi za jirani, mfano nchi kama Kenya, imetenga shilingi bilioni ishirini na sita kwa ajili ya Kenya Tourist Board, South Africa imetenga shilingi bilioni 60, Namibia wametenga shilingi bilion 20, Uganda yenyewe, nchi ndogo kama Uganda imetenga shilingi bilioni nane kwa ajili ya kutangaza utalii. Sasa hapa kwetu tutautangazaje utalii bila kuiwezesha TTB?

Mheshimiwa Spika, 2.8 billion Mheshimiwa Spika, tunazungumzia watalii kuwa wengi, Mheshimiwa Waziri amesema watalii wa Tanzania wamefika 1.3 million ambao wamekuja kuitembelea Tanzania. Lakini, Kenya pamoja na matatizo na waliiondoa VAT lakini watalii wa Kenya wamekuwa ni wengi kuliko Tanzania, walikuwa milioni milioni na laki nne.

Mheshimiwa Spika, sasa kama ni mambo yale unayosema ya VAT haiku-affect Tanzania naomba mkakae mfanye tathmini upya, muangalie kweli kama VAT haiku- affect utalii wa Tanzania kwa sababu ile VAT iliyoongezeka ukiangalia zile fedha za mwaka juzi hiyo piece iliyoongezeka ni ile VAT 18% iliyoongezeka, kwa hiyo mapato hayajaongezeka. Kwa hiyo, naomba mlitathmini upya suala zima la VAT katika utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine kwenye masuala ya wafanyabiashara wa utalii ni hizi tozo, mlolongo wa tozo. Unakwenda kwenye ofisi ya mtu unakuta imepambwa na certificate nyingi tu, wafanyabiashara hawakatai kulipa kodi lakini tunaomba mfanye basi iwe dirisha moja, maana time is money huwezi kumchukua mfanyabiashara anatoka ofisi hii anaenda ofisi hii, mnampotezea muda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ikiwa ni kwenye dirisha moja, watalipa hizo kodi. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri tunaomba sana mfanye iwe ni kwenye dirisha moja na wafanyabiashara watalipa hizo tozo kwenye dirisha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kitu nimekuwa nikizungumzia hapa mara nyingi kuhusu volunteers. Kuna hawa wanafunzi wanatoka nje, they are just 16/14 years old, wanakuja wazazi wao wanakusanya pesa kule kwenye nchi za nje wanakuja wanafanya community work, wanajenga mashule, wanajenga madarasa, mabwalo na kila kitu. Kazi ya hawa wanafunzi wanakuja kama wiki mbili, wanakuja wanapiga rangi, wanajenga madarasa lakini wanatumia mafundi watanzania wao wanataka tu ile adventure. Lakini unakuta Serikali naomba na Wizara ya Mambo ya Ndani mnawa-charge dola 500 za kufanya kazi pamoja na dola 50 za tourist visa, lakini wale watoto hawafanyi kazi wakija Tanzania wanafanya hiyo community work kwa siku saba lakini wanaenda kupanda Mlima Kilimanjaro, wanaenda Ngorongoro wanaenda Serengeti mpaka Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hii, kazi hiyo wanaofanya ni part of tourism sasa badala ya kuwa-encourage kwamba waendelee na hiyo part of tourism ambayo tumeianzisha, sasa mnawafanya wanaacha wengine wamehamia Mombasa kwa sasa hivi. Kwa hiyo, Mombasa wamewapokea na wanafanya hizo community work kule, kule Moshi wamejenga shule nyingi tu lakini sasa hivi wame- cancel zile booking wanaenda Mombasa.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba uliangalie hilo ili muweze kuwafanya hawa wafanyakazi warudi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipoongelea Mlima Kilimanjaro kila siku tunaonga hapa kuhusu Mlima Kilimanjaro. Mlima Kilimanjaro unaiingizia mapato Serikali mapato mengi sana, lakini bado tumeshauri mara nyingi ili kulinda mazingira kwa kuanzia tu, tunaomba ile njia ya Machame route mjenge mahema kwa ajili ya kulia mess tents, nataka nijue pamoja na vile vyoo kutoka Ujerumani vilikuwa vya majaribio chemical toilets vimefikia wapi.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Deni la Taifa, Wizara hii ndiyo yenye jukumu la kusimamia Deni la Taifa. Mwaka 2017/2018 limezidi kuongezeka kwa dola za Kimarekani milioni 1,054.6 sawa na shilingi 2,320,120,000,000 kutoka USD milioni 19,957.6 sawa na 43,906,720,000,000 mwaka 2016. Hii
inatokana na taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania. Deni hili kubwa husababisha Serikali kulipa riba kubwa na kurudisha shughuli za maendeleo nyuma na kudumisha uchumi wa nchi. Deni hilo sio himilivu tena kwa sababu linaelekea kufikia nusu ya Pato la Taifa. Serikali ije na kutueleza ina mikakati gani ya kupunguza deni hilo badala ya kuendelea kukopa mikopo ya kibiashara yenye riba nafuu na kuendeleza kuongeza Deni la Taifa?

Mheshimiwa Spika, kuhusu utendaji wa TRA, ni vizuri wafanyakazi wa TRA wakatoa elimu kwa wafanyabiashara jinsi ya kulipa kodi badala ya kufanya kama wanakomoa wafanyabiashara. Je, ni kwa nini walimbikize mahesabu kwa zaidi ya miaka kumi ndiyo wafanye auditing? Halafu wanatoa fine za hali ya juu wakati biashara pengine haina hata mtaji wa kutosha na kusababisha biashara nyingi kufungwa kwa kukosa fedha. Kwa hiyo, hayo malimbikizo ya kodi hayana afya kwa wafanyabiashara na ieleweke wafanyabiashara hawakwepi wala hawakatai kulipa kodi, wapewe elimu, kitendo cha kuviziana na kuvamiana kwenye biashara ndicho huwasababisha baadhi ya wafanyabiashara kufikiria wananyanyaswa na kuonewa.

Mheshimiwa Spika, ni wakati sasa Serikali kuangalia haya matumizi ya EFD machine yanatumika vizuri na ziwe zinafanya kazi. Zaidi ya siku kumi mashine hizi nchi nzima zilikuwa hazifanyi kazi na kusababisha wafanyabiashara kushindwa kutoa receipt. Si hilo tu pia receipt hizi huwa zinafutika. Ni kwa nini kusiwe na mashine zinazoweza kudumu? Pia mashine hizo bei yake ni ghali sana kwa baadhi ya wafanyabiashara wadogo wadogo, shilingi 700,000 hadi 650,000 ni nyingi sana. Ili Serikali iweze kupata mapato kwa kila mfanyabiashara ni vizuri Serikali ikagharamia mashine hizo ili kila mtu aweze kulipa kodi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu matumizi ya fedha za kigeni nchini, fedha yetu ya Tanzania shilingi kama nchi tunachangia kwa thamani yetu kushuka. Je, ni kwa nini taasisi za Serikali zinapokea malipo kwa dola za Kimarekani? Mfano, malipo yote ya hifadhi mfano, Kilimanjaro, Serengeti na kadhalika lazima kulipia kwa dola. Nchi jirani zote na zingine duniani ni lazima kubadilisha fedha hizo kwenye maduka ya fedha na kulipa kwa thamani ya fedha ya nchi husika. Lakini hapa kwetu ni tofauti kabisa. Je, ni lini sasa Serikali itaziagiza taasisi hizi kuanza kupokea Tanzanian Shillings? Tusipothamini fedha zetu nani atazithamini?
Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Spika, umiliki wa vitalu vya uwindaji, tamko la Serikali la tarehe 23 Januari, 2017 kuwafutia wamiliki wa vitalu vya kuwindia biashara kutoka miaka mitano hadi miwili kumesababisha biashara hii kuyumba. Biashara ya utalii wa uwindaji huwa inaandaliwa kwa muda mrefu sana na uwekezaji wake ni wa gharama ya juu inayohusu kukarabati miundombinu mbalimbali. Aina hii ya utalii ni ya bei ya juu, sasa ni karibia dola 60,000 mpaka dola 80,000 kwa mtalii kuja kwenye utalii huu. Hivyo watalii wanataka wawe na uhakika wa deposit zao watakazotoa. Pamekuwa hakuna utulivu tena katika tasnia hii. Wawekezaji hawana uhakika na biashara zao hadi kupelekea wengine kuvirudisha vitalu hivyo.

Mheshimiwa Spika, ushauri, kama Serikali inataka kuuza kwa mnada hivyo vitalu kwa nini visiuzwe na vile vilivyo wazi kama jaribio kulikoni kuvuruga wawekezaji ambao tayari wameshatumia fedha nyingi kuendeleza vitalu vyao?

Mheshimiwa Spika, sekta ya utalii inachangia katika pato la Taifa asilimia 17.5 na inaweza kuchangia vizuri zaidi kama tukiweza kuendeleza Southern Circuit, utalii wa utamaduni na michezo kwa mfano Kilimanjaro International Marathon inakuwa ni kivutio kikubwa sana mbali na riadha, watu wakimaliza kukimbia huenda kupanda Mlima Kilimanjaro na kutembelea mbuga zetu lakini wengi wanarudi zaidi ya mara moja. Lakini safari ya kwenda Selous lakini tour ya kwenda huko ni ghali sana, hakuna hoteli za kutosha na zilizopo ni za ghali sana.

Mheshimiwa Spika, katika sekta hii kumekuwepo na tozo nyingi sana takribani tozo 36 tofauti. Wafanyabiashara hawakatai kulipa kodi lakini kwa nini zisiunganishwe zikalipwa sehemu moja ili kuondoa usumbufu hata dakika moja tu ya mfanyabiashara ni fedha. Unakuta ofisi ya mtu (tours operation) imezungukwa na leseni nyingi kama mapambo.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hivi bado Serikali haijaelekeza ipasavyo katika utalii wa picha, mfano kuna baadhi ya watalii wanataka wafanye utalii wa kupiga picha wakati wakipanda mlima, lakini huu ukiritimba uliopo mpaka apate kibali cha kupiga picha ni shughuli, havitoki kwa wakati mpaka mtalii huwa ana-concel safari yake.

Mheshimiwa Spika, Mlima Kilimanjaro; Serikali kwa kushirikiana na nchi ya Ujerumani walikuwa waweke clinical toilet katika njia za kupanda Mlima Machame, Umbwe route, Lemosho, Landorosi lakini mpaka leo Serikali haijaweza kuviweka vyoo hivyo. Je, ule mchakato umeishia wapi? Hii inasaidia sana kutunza mazingira (usafi) sababu kule crater kunatia aibu ni kuchafu sana.

Suala lingine mara nyingi nimekuwa nikishauri kwa kuanzia ile njia ya Machame KINAPA wajenge majiko ya kupikia na sehemu za kulia (dinning tent), hii itasaidia sana kuanza tu uniformity na kuzuia kila kampuni kuchimba sehemu tofauti kuweka mahali pa kulia na kupikia na hii itavutia sana watalii kwa kuona park fee wanazolipa zimetumika kwa kuendeleza park hiyo ukizingatia ilikusanywa zaidi ya bilioni 20 hizi ni Mlima Kilimanjaro tu.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kilimanjaro, Jimbo la Moshi Vijijini, Kata ya Mbokomu wenyeji waligundua mti mrefu sana na unakisiwa una ziadi ya miaka 500 mpaka leo sijaona juhudi zozote za Serikali kwenda kuhifadhi sehemu ile kuweka uzio ili watalii waanze kuutembelea officially na Serikali wanapeleka watalii pale anatoza asilimia ngapi kutokana na mti huu?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Idara ya Zimamoto; katika Jiji letu la Dar es Salaam panakuwepo na ongezeko kubwa la majengo na yaliyojengwa karibu sana na majengo mengine ni marefu sana. Pindi linapotokea janga la moto tumeshuhudia sehemu nyingi nchini magari hayo huwa yanaishiwa maji. Pili, kwa majengo marefu yaliyopo Dar es Salaam ni magari mangapi yanayoweza kutoa huduma ya kuzima moto mfano ghorofa ya mwisho kabisa ni ya ngapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dodoma kwa sasa hivi ni Jiji na patakuwepo na ongezeko kubwa la watu na majengo je, Serikali imejipangaje kuongeza magari ya zimamoto Dodoma na nchi nzima na yawe ya kisasa na yenye vifaa vyote vya kuokolea maji, ngazi ndefu, chopa na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu makazi ya kuishi Askari Polisi; Askari hawa wanafanya kazi katika mazingira magumu. Mfano Askari wa Barabarani unawakuta wapo barabarani siku nzima wengine kujificha vichakani kuvizia madereva wanaoendesha magari kwa mwendo unaopita limit kupelekea kuhatarisha maisha yao. Hivyo, wakirudi nyumbani wanatakiwa wakute makazi mazuri waweze kupumzika na familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kusikitisha hata hapa katika Jiji la Dodoma bado zile nyumba za bati kuanzia juu mpaka chini (full suit) bado zipo Dodoma na Askari wetu wanaishi kule. Tukumbuke hali ya hewa hapa Dodoma ilivyo na joto halafu watu waishi kule. Bado vyoo ni vya kuchangia, kichumba kidogo na wana familia, huu si utu kabisa. Je, Serikali ina mikakati gani ya kuwajengea makazi yenye hadhi kwa Askari wetu kwa kuanzia na hapa Dodoma?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Askari wa barabarani (Traffic) watumie muda mwingi zaidi kutoa elimu kwa madereva na watumiaji wa barabara, madereva wa bodaboda, baiskeli hata watembea kwa miguu; ajali nyingi zinatokea tu kwa sababu wengi hawajui sheria za barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha kuona Askari wetu wakitumika kama wakusanya mapato badala ya kufanya kazi zao za msingi. Kazi za ukusanyaji mapato zifanywe na idara husika na hatuwezi kuendesha nchi kwa faini za magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hali ya amani nchini; pamekuwepo na matukio ya uhalifu unaofanywa na watu wasiojulikana mfano watu wanauawa, kuokotwa katika fukwe za bahari Coco beach Dar es Salaam, watu kutekwa na kuteswa na tukio la hivi karibuni lililotokea huko Tarime kwa kijana Chacha kupigwa kisu na Askari Polisi hadi kufariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki ni kitendo cha kulaani sababu raia hata wahalifu hukimbilia Polisi wakijua ndiko wanakwenda kwenye mikono salama lakini haikuwa hivyo. Ni hatua gani Jeshi la Polisi imemchukulia Askari huyo ili lisitokee sehemu nyingine? Je, ni lini Jeshi litatoa report hizo maiti zinazookotwa zinatokea wapi na uchunguzi unaonesha maiti hizo zilifanyiwa nini hadi kufariki (cause of death). Ni vizuri wananchi wakafahamishwa kinachoendelea ili utulivu uliopo usije ukaharibu amani tunayoiimba ambayo kwa sasa haipo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza kuongelea kuhusu utawala bora. Utawala bora ni nini? Je, nchi yetu inazingatia utawala bora? Tumeona matukio mengi hapa nchini yasiyokidhi utawala bora wenye kufuata sheria na kujali haki za wananchi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, uhuru wa kutoa maoni na kupata habari. Hii ni moja ya msingi wa utawala bora kwa wananchi kupata habari lakini tumeona kwa sasa Serikali imezuia hata wananchi kufuatilia majadiliano yanayoendelea ndani ya Bunge (live on TV). Baadhi ya waandishi ya habari wamekuwa wakipotea, wengine kupigwa na baadhi ya magazeti kufungiwa kisa ni kwa kutoa maoni yao dhidi ya Serikali. Hata vyama vya siasa vilivyoanzishwa kisheria kwa Sheria Na.5 ya mwaka 1992 bado haviruhusiwi kufanya mikutano ya hadhara ili kuwaeleza wananchi sera zao badala yake viongozi wengi wa upinzani wamekuwa wakifunguliwa mashtaka kwa kisingizio cha uchochezi. Je, huu ndiyo utawala bora?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ukiukwaji wa haki za raia. Sasa hivi katika nchi yetu panakuwepo na kundi la watu wasiojulikana wanaoteka watu. Mara nyingi watu wamekuwa wakiokotwa pembezoni mwa bahari ya hindi wakiwa wamefariki. Mfano, Mwandishi wa Gazeti la Mwananchi, Ndugu Azovi Gwanda na Msaidizi wa Mwenyekiti wa CHADEMA, Ndugu Ben Sanane, mnadhimu wetu wa Kambi ya Upinzani, Mheshimiwa Tundu Lissu alipigwa risasi mchana kweupe lakini mpaka leo Serikali haijatoa taarifa yoyote kuhusu matukio hayo yanayoendelea hapa nchini. Je, usalama wa raia uko wapi hapa nchini? Ni lini Serikali itatoa maelezo ya kina juu ya hatua iliyofikia katika kukomesha matukio haya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ajira. Utawala bora ni pamoja na kuwaongezea watumishi mishahara lakini kwa miaka miwili sasa watumishi hawajaongezewa mishahara kama sheria inavyoelekeza. Huu siyo utawala bora kabisa. Hii ni pamoja na kuwapandisha madaraja watumishi wa umma kwani haijafanyika kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niongelee Ofisi ya Rais, TAMISEMI kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za maendeleo kutoka kwa wakati katika Halmashauri; fedha za maendeleo kutoka Serikali Kuu haziendi au hazitumwi kwa wakati kwenda kwenye Halmashauri na kupelekea Halmashauri kushindwa kutekeleza miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe siku za nyuma Halmashauri zilikuwa na vyanzo vya mapato vya kukusanya kodi za ardhi na ada mbalimbali ambazo zote hizi zinakwenda Serikali Kuu. Ni vizuri sasa katika makusanyo hayo Halmashauri zikate asilimia 30 ya makusanyo ili zibaki kwa ajili ya maendeleo. Halmashauri nyingi zimeshindwa kutenga hata zile asilimia10 kwa ajili ya vijana, akinamama na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu; ili mwanafunzi aweze kufaulu vizuri na Mwalimu akubali kufundisha bila kuchoka ni lazima mazingira ya kufundishia na miundombinu ya kufundishia iwe mizuri. Tumeshuhudia shule nyingi tukianza na shule za awali, nyingi hazina Walimu wa kutosha, hakuna nyumba za Walimu, zaidi vijijini, hakuna Walimu wanataka kwenda huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba wa Walimu wa hisabati na sayansi ni mkubwa takribani 22,460 ni pungufu na shule za msingi ni takribani 186,003 ni pungufu sawa na asilimia 83.1. Serikali ina mikakati gani ya kuhakikisha upungufu huu unajazwa kwa kuajiri Walimu? Baada ya hayo ni lazima Serikali ihakikishe:-

(a) Walimu wanalipwa posho zao;

(b) Pawepo na mashimo ya vyoo ya kutosha; na (c)Maabara zikijengwa ihakikishwe zina vifaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya; Serikali imekuwa ikitoa kauli ya kujenga zahanati na vituo vya afya katika kila kijiji na kata lakini ikumbukwe kuna zahanati zilizopo lakini bado zina upungufu mkubwa, hazina Wauguzi wa kutosha, dawa hazipelekwi kwa wakati, hazina ambulance ya kupeleka mgonjwa aliyezidiwa pengine anahitaji rufaa kwenda ngazi ya juu. Mfano, kutoka zahanati kumkimbiza hata hospitali ya Wilaya wanashindwa na mara nyingine kupelekea wagonjwa kufariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo la kusikitisha mahali kama Moshi Manispaa hakuna Mfamasia, aliyepo ni technician tu, hivi huyu anaendaje kukagua Mafamasia walio juu yake kitaaluma?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo; katika Hamashauri yetu bado kilimo hakijathaminiwa ila Serikali imekuwa ikija na mbwembwe za maneno tofauti kama vile kilimo ni uti wa mgongo, kilimo kwanza na kadhalika, lakini kilimo bila watalaam hakiwezi kuwa na tija. Kuna uhaba mkubwa wa Maafisa Ugani na uhaba wa pembejeo. Mfano, sasa hivi mbolea ni ghali sana mfuko Sh.53,000, mkulima wa kawaida anaweza kununua? Hata wakilima na kufanikiwa kuna uhaba mkubwa wa kuuza mazao yao. Sasa hivi mbaazi ziko tu nyumbani kwa wakulima na mahindi mengi yanaharibika na hata wakulima wakitaka kuuza nje Serikali inazuia na hata wakitaka vibali ni ngumu kuvipata.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nami nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa pumzi niweze kusimama katika Bunge lako Tukufu na kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee naomba niipongeze hotuba ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, iwapo hakuisoma lakini naamini kwamba Serikali imesoma na mmeona imefanyiwa utafiti wa kutosha, imesheheni ushauri wa kutosha, nategemea mtaifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie barabara ambayo nimekuwa nikiizungumzia kila leo, barabara iliyopo Moshi Vijijini kutokea Kibororoni kwenda Kikarara hadi Tuduni. Kweli kwa sasa hivi Serikali imetenga fedha, imetengeneza kwa kiasi fulani, lakini haifiki hata kilomita moja. Tunajua sasa hivi kule Moshi masika inaenda kuanza, kwa hiyo, ni mategemeo yangu barabara ile watatengeneza mitaro na ninaomba bajeti ya mwaka huu basi zile kilomita 10 zilizobaki Serikali itenge fedha iweze kuimaliza kwa sababu nimeshaelezea umuhimu wa barabara ile ni barabara ambayo ni ya kitalii na KINAPA imeitenga ile barabara kwa ajili ya watu mashuhuri ambao watakuwa wanapanda mlima kwa kupitia barabara ya Old Moshi. Kwa hiyo, ni mategemeo yangu sasa bajeti ya mwaka huu barabara ile itatengewa fedha za kutosha ili iweze kumalizika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie TEMESA. Serikali imekuwa ikinunua magari ya kifahari kila mwaka na TEMESA zilijengwa kila mkoa kwa lengo la kuhakikisha kwamba gari zote za Serikali zinatengenezwa kwenye karakana za TEMESA. Mashine zilizoko kule TEMESA kwa sasa hivi zimepitwa na wakati, hazifanyi kazi na magari ya kisasa sasa hivi hayawezi kutambulika na zile mashine zilizoko TEMESA kwa sababu teknolojia sasa hivi ni mambo ya kompyuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nategemea sasa Serikali ili kupunguza matumizi itengeneze zile karakana zilizoko kwenye kila mkoa na kuhakikisha kwamba wanaweka vifaa vya kisasa ili kupunguza matumizi, maana yake sasa hivi unakuta Serikali inatengeneza gari inapeleka gari TEMESA, TEMESA wanachukua wanapeleka kwenye private garage ambazo ni za Wachina, wao wanaenda kupeleka bili inakuwa mara tatu ya bili ambayo ingetengenezwa na TEMESA. Kwa hiyo, naishauri Serikali ipeleke mafundi wetu waende wakasomee jinsi ya kutengeneza haya magari na mlete sasa teknolojia mpya ambazo zitaweza kutumika katika hizo garage ili tuweze kupunguza matumizi kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inaenda sambamba na karakana iliyoko Kilimanjaro. Kweli tumenunua ndege nyingi na tunahitaji hizo ndege, lakini tukitengeneza ile karakana iliyoko pale KIA ina maana ndege zetu zitaweza kutengenezwa pale pale KIA. Badala ya kupeleka ndege Canada mnaweza mkawaambia wale mafundi kutoka Canada wakaja wakatengeneza ndege pale KIA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili ni jambo ambalo tumekuwa tukilizungumzia mara nyingi sana, tunarudia na kurudia lakini bado Serikali haijaona umuhimu wa kutengeneza ile karakana. Nataka sasa Mheshimiwa Waziri akija atueleze, kwa jinsi gani mmejipanga kuhakikisha kwamba mnaitengeneza ile karakarana kwa sababu sasa hivi kama nchi tumeanza kuwa na ndege zetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni pamoja na uwanja wa Moshi Airport. Uwanja wa Moshi Airport idea ilikuwa ni kufanya ule uwanja uwe kwa ajili ya mafunzo ya ma-pilot. Sasa hivi na sisi tunasema tuna ndege nyingi, ule uwanja sasa umesahaulika kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishawahi kuzungumza kipindi kilichopita na ninarudia tena, ule uwanja watu wengi sasa hivi wanalima maharage kule na karanga. Ni aibu. Uwanja ni mzuri kabisa, ulikuwa unatumika, lakini sasa hivi una potholes haufahi kabisa, hata ndege ndogo sidhani kama zinaweza kushuka pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujibu hapa atuelezee sasa wana mikakati gani ya kuhakikisha kwamba Moshi Airport inatengenezwa na iwe kwa ajili ya mafunzo ya ma-pilot? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Kilimanjaro tuna zile mbio za Kilimanjaro Marathon. Mbio hizi zimekuwa zikikua mwaka hadi mwaka. Mfano, mwaka 2014 walikuwa wakimbiaji karibu 4,000; mwaka 2015 wakapanda zaidi wakafika 7,000; mwaka 2018 wamefika 9,000; na mwaka huu
2019 wako zaidi ya 12,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbio hizi zinafanyika katika uwanja wa Ushirika na uwanja huu unalemewa kwa sababu watu ni wengi. Pale Moshi tuna ule uwanja wa Kim Memorial. Uwanja ule una michezo zaidi ya saba, lakini pale kuna soko la mitumba. Sijakataa watu wa mitumba wawe pale, wanaweza wakawepo pale mkawatengea sehemu lakini bado ile sehemu kubwa iliyobaki ikatumika kwa ajili ya michezo. Kama tunavyosema michezo ni afya, lakini watu wa Kilimanjaro hatuna mahali pa kufanya michezo na tunajua magonjwa ya kuambukiza sasa hivi yamekuwa ni mengi na magonjwa ya kuambukiza tunaweza tukajikinga nayo kwa kufanya mazoezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni mategemeo yangu sasa Serikali itatusaidia watu wa Kilimanjaro ule uwanja uweze kutumika sasa maana mwaka unaokuja sasa 2020 ina maana hizi mbio kwa sababu zimezidi kujitangaza watu wanaweza wakafika hata 15,000 na wakifika hivyo, siyo kwamba wanakuja kukimbia tu, wanaleta biashara Moshi, hoteli zinajaa mpaka Arusha na wakija siyo kwamba wanakimbia tu, wanapanda mlima, wanaenda safari, kwa hiyo, inaongeza pato la Taifa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kidogo kuhusu uwekezaji. Kiongozi wa Kambi ya Upinzani katika katika hotuba yake ukurasa wa 30 amezungumzia vizuri sana kuhusu uwekezaji. Sasa hivi imekuwa ni kero kwa mtu kuja kuwekeza Tanzania. Kodi ni nyingi sana. Ameainisha hapa kodi zote ambazo zinatakiwa mtu alipe akija kufanya biashara Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ku-declare, mimi pia ni mfanyabiashara. Wafanyabiashara wengi wanafunga biashara kwa sasa hivi, kisa tu kodi. Hawakatai kulipa kodi, lakini zile kodi basi ziwe rafiki. Unakuta mfano, OSHA; OSHA yenyewe unakuta inampa mtu bili ya shilingi zaidi ya shilingi 2,400,000, hujaenda TBS; hujalipa withholding tax; hujalipa income tax; kodi ni nyingi mno. Hebu jaribuni kufanya hizi kodi ziwe rafiki na mtapata kodi nyingi zaidi na Serikali itapata mapato zaidi. Kwa namna hii, ukienda kuangalia ni wafanyabiashara wangapi wamefunga biashara, ni wengi sana. Kwa hiyo, nafikiri kuna haja ya kuja kuleta sheria hapa na kubadilisha sheria zetu za kodi ndiyo solution pekee ambayo tunaweza tukabadilisha mfumo wetu wa kodi hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kidogo kuhusu kilimo. Tunasema kilimo ni uti wa mgongo, maneno mengi tu yamekuja. Tunajua kwamba asilimia zaidi ya 80 ya Watanzania ni wakulima, lakini katika hotuba ya Kambi ya Upinzani tumeeleza wazi kabisa 2016/2018 Serikali ilitakiwa itenge shilingi 150,253,000,000/= kwa ajili ya fedha za maendeleo, lakini hadi Machi, 2018 zimetoka tu shilingi bilioni 16.5 sawa na asilimia 11. Hivyo zaidi ya asilimia 89 ya fedha za maendeleo kwa ajili ya kilimo hazikutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama kweli tunataka kuendeleza wakulima wetu, tunasema tunataka Tanzania ya Viwanda, bila kilimo hivyo viwanda tutavitoa wapi? Unakuta tunahitaji watafiti, tunahitaji mbegu ambazo ni za kisasa. Kwa fedha hizi ambazo Serikali imetoa, sioni ni jinsi gani ambayo tunaweza tukaendeleza kilimo hiki. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Matumizi ya mifuko ya plastic; ni jambo jema kwa Serikali kutoa tamko mwisho wa kutumia mifuko ya plastic ni 1/6/2019. Tamko pekee halitoshi, ni vizuri Waziri atueleze ni lini suala hili litatumika kisheria ili yeyote anayetumia mifuko hiyo ajue kuna faini ya kulipa au anaweza kufungwa jela. Bila sheria kuna baadhi ya watu wataendelea kutumia mifuko hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona kabisa mwaka huu mvua mfano kaskazini bado hazijanyesha lakini kwa kisingizio cha mabadiliko ya tabianchi, lakini ni wazi kuwa miti imekuwa ikikatwa ovyo kwa matumizi ya mkaa, wengine kwa ajili ya kilimo. Siku zilizopita vijijini (Serikali za Vijiji) ilikuwa ni lazima kupanda miti na ilikuwa hairuhusiwi kulima kando ya mito, lakini sasa hivi ni jambo la kawaida kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri shule zote za msingi na sekondari katika kila vijiji wawe na vitalu vya kupanda miti na iwe kabisa ni elimu kuanzia shule za awali kuhusu umuhimu wa kutunza mazingira kwa kupanda miti na wajue ukikata mti lazima uwe umepanda mti mwingine. Wazee wetu walisomesha vijana wao kwa kukata mti na kuuza mbao lakini walihakikisha kuna mti mwingine pembeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri kila halmashauri ziwe na vitalu vya miti ikiwezekana ya matunda pia ambayo yatatumika kujenga afya na kuongeza kipato kwa wananchi na uuzwe kwa bei nafuu ili kila mwananchi aweze kununua.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Michezo, kama tujuavyo ni afya, ni furaha na yanaleta upendo. Duniani pote magonjwa yasiyoambukiza kama shinikizo la damu la kupanda na kushuka, ugonjwa wa kisukari na magonjwa ya moyo huepukika mapema kwa kufanya mazoezi, lakini hapa Tanzania Halmashauri nyingi hazina viwanja vya michezo na pia barabara zetu sio rafiki kwa watu kufanyia mazoezi, hakuna sehemu za watembea kwa miguu.

Je, kwa nini Serikali isikae chini ili Wizara hii na Wizara ya Miundombinu wakaweka mikakati iwe ni lazima wanapojenga barabara wahakikishe kuwepo na sehemu za wapita kwa miguu ili iwawezeshe wananchi kutembea?

Mheshimiwa Spika, vile vile ni vizuri katika sehemu za kazi pawepo na sehemu za kuogea ili wafanyakazi watembee kwenda kazini, wakifika ofisini wanaoga.

Mheshimiwa Spika, viwanja vyote vilivyotekwa na CCM katika kila Halmashauri virudishwe kwenye Halmashauri kwa kuwa vilikuwa ni vya Umma na wananchi wote wavitumie kwa ajili ya mazoezi.

Je, Serikali ina mpango gani kwa kukifufua kiwanja wa King Memorial kilichopo Mkoani Kilimanjaro katika Manispaa ya Moshi ili kianze kutumika? Ukizingatia kiwanja kile kina michezo zaidi ya saba lakini kipo tu pale wananchi wanapanda maharage wakati kiwanja kipo.

Mheshimiwa Spika, kulikuwepo na mchakato wa ku- design vazi la Taifa na fedha zilitumika kwa ajili ya vazi hilo, lakini hadi leo hatujapata mrejesho, zoezi hili lilifikia wapi? Je, ni lini mchakato wa vazi la Taifa utakamilika?

Mheshimiwa Spika, ni haki ya wananchi kupata habari lakini ni jambo la kusikitisha vyombo vya habari havipo huru na vimebanwa sana. Local channel za television tulielezwa zilitakiwa ziwe bure, lakini cha kusikitisha ni chombo kimoja tu cha TBC ndicho kinachotoa matangazo tena kwa upendeleo, hawatoi habari zote. Mfano, hata hotuba za Upinzani Bungeni hazijawahi kutangazwa na TBC.

Mheshimiwa Spika, magazeti hayana uhuru. Yakiandika ukweli huwa yanapewa adhabu ya kufungiwa. Je, huu ndiyo uhuru wa habari mnaoutangaza?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Spika, Madaktari wa Mifugo. Kumekuwepo na upungufu mkubwa sana wa madaktari wa mifugo na kupelekea mifugo kufariki bila ugonjwa kutambulika na kueneza magonjwa hovyo. Pia kumekuwepo na kutopatikana kwa dawa za mifugo. Kwa mfano, unakuta kuna ugonjwa wa kichaa cha mbwa na chanjo hazipo na madaktari wa mifugo hawapo. Je, Serikali ina mikakati gani ya kuhakikisha madaktari wa mifugo na dawa zinapatikana? Siku za nyuma, madaktari walikuwa wanatembelea wafugaji na kutoa chanjo. Je, ni lini utaratibu huu utarudi?

Mheshimiwa Spika, sekta ya mifugo; wafugaji wengi wanajitahidi sana kufuga kisasa na kuzalisha maziwa mengi ambayo yangeweza hata kuuzwa nje, kutengeneza cheese, siagi na kupata nyama; lakini tatizo bado Serikali haijaweza kushirikiana kati ya Wizara na Wizara. Kwa mfano Wizara ya Mifugo kujenga viwanda vya maziwa ili kuweza kuwapatia wafugaji masoko. Je, nchi kama Tanzania kuna sababu ya kununua maziwa, siagi, cheese kutoka nchi za nje? Ardhi tunayo, mifugo tunayo, wafugaji wapo shida ni nini?

Mheshimiwa Spika, Ushauri; Serikali ijitahidi kila sehemu yenye wafugaji ihakikishe inajenga majosho ya kutosha ili wakati wa kiangazi mifugo isife kwa kiu; na ni vizuri kufanya hili katika kila Wilaya.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na kuwa mtu wa kwanza katika mjadala wa leo. Wizara ya Viwanda na Biashara katika fedha za maendeleo mwaka 2018/2019 walitakiwa watengewe shilingi bilioni 100.02 lakini zilizotolewa ni shilingi bilioni 13.63. Mwaka 2019/2020 fedha za maendeleo zilizotengwa zilikuwa ni shilingi bilioni 51.5 pungufu ya asilimia 48.7 ya zilizotengwa za mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutotoa fedha za maendeleo za kutosha inachangia kutokuziwezesha taasisi ambazo ziko chini ya Wizara kama CAMARTEC, TIRDO na SIDO ili kuweza kufanya tafiti za kuweza kuendeleza vifaa vya kilimo au vifaa vya kwenye viwanda. Kwa hiyo naishauri Serikali itenge fedha za kutosha ili waweze kuendeleza shughuli za viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la viwanda vilivyoko katika Mji wa Moshi. Moshi tuna viwanda vingi sana, kulikuwa na Kiwanda cha Kibo Match ambacho kilikuwa kinatengeneza vibiriti, lakini kiwanda kile mpaka leo hii kimekufa na hakijaendelezwa kwa vyovyote vile. Kiwanda kile kilikuwa kinazalisha ajira zaidi ya 600 na walikuwa wanazalisha vibiriti zaidi ya 6,000, lakini kwa sasa hivi ina maana ajira zile zimepotea na vijana wanazurura mtaani wakati kiwanda kipo pale gofu, ambapo Serikali ingeweza kuvifufua na kikafanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kingine ni kile cha ngozi kilichoko Moshi, kinatengeneza ngozi ndiyo, lakini kwa kiwango kidogo sana. sijui ni kwa jinsi gani Wizara imeenda kuangalia suala zima la mazingira kwa sababu pale wakazi wa Pasua, Mabogini, Bomambuzi wanaanthirika sana na harufu ya ngozi inayotoka katika kiwanda cha ngozi. Sasa sijui kma wameshafanya utafiti kugundua kama ile harufu inayotoka katika kiwanda kile kama inadhuru watu au la. Ningeomba Serikali ifanye utafiti iende ikaangalie suala zima la mazingira katika kile Kiwanda cha Tanneries. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo kulikuwa na kiwanda cha magunia, mpaka leo ni gofu liko pale. hakuna chochote kinachoendelea, imekuwa ni mahali pa kuhifdhi tu vitu lakini hakuna kiwanda cha magunia pale Moshi. Sasa sijui mpaka leo hii bado tunaimba kuhusu viwanda vya magunia Moshi wakati katani zipo lakini sijui kwanini sasa viwanda vile havifufuliwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kingine kilichoko katika Mkoa wetu wa Kilimanjaro ni kiwanda mama cha machine tools. Tumekuwa tukipiga kelele kila siku. Kiwanda kile bado hakizalishi, vipuli vilivyoko pale ni teknolojia zile za zamani kwa hiyo wanashindwa kuzalisha viwanda kwa ajili ya viwanda vidogo vidogo. Sasa sijui lini sasa Serikali itafanya ule utafiti iliyosema inafanya na kutafuta mwekezaji ili watengeneze teknolojia mpya, wazalishe viwanda vidogo vidogo ili viweze kusaidiana na SIDO watu waweze kuzalisha na mazao yao wakiwa kule kule vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuulizia kuhusu kiwanda cha General Tyre Arusha. Kiwanda kile kilikuwa kinafanya kazi na kilikuwa kinazalisha matairi mazuri East na Central Africa kabisa lakini sasa mpaka leo hii ni zaidi ya miaka kumi tumekuwa tukikizungumzia kiwanda cha General Tyre kilikuwa kimeajiri watu wengi sana lakini bado Serikali haijaonesha ni lini sasa kiwanda kile kitaanza kwa sababu bado tuna yale mashamba yaliyoko kule Tanga ambayo yanazalisha mpira, yamekaa tu kule badala yake wamekuwa Wakenya wakienda kule wanaenda kuchukua zile rubber wanaenda kutengeneza big Nairobi na sisi ambao tungeweza kutumia ile rubber kwa ajili ya kwenda kutengenezea matairi yetu kule Arusha. Lakini mpaka leo hii Serikali haijasema ni lini sasa kiwanda cha General Tyre kitaanza kazi. Tunaomba watupe time frame ni lini kitaanza kazi ili vijana wetu waweze kupata ajira kwa sababu kiwanda kile kina nafasi ya kutosha, kimelala tu pale, vijana wanazurura lakini wangeweza kupata kazi katika kiwanda kile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kidogo nizungumzie kuhusu masoko. Mkoa wa Kilimanjaro tunalima sana ndizi na tunalima pia maparachichi. Lakini unakuta wakulima wanavuna maparachichi kwa wingi sana lakini yote yanaoza kwa sababu tu hawana masoko na wengine ni kwa sababu ya packaging na mengine unakuta…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Lucy Owenya kwa mchango wako.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi. Nipende kuipongeza Kambi ya Upinzani kwa hotuba yake nzuri pamoja na ile ya Kamati. Nategemea Mheshimiwa Waziri atachukua maoni yale na kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitajikita zaidi katika Sekta ya Utalii. Kwenye report nyingi tumeona kwamba, sekta hii ni kati ya sekta inayochangia katika pato la Taifa kwa asilimia 17.5 na asilimia 25 kwa fedha za kigeni, lakini naona Serikali bado haijaichukulia seriously hii sekta ya utalii. Kwa mfano kwenye fedha za maendeleo ziliidhinishwa shilingi bilioni 26.8, lakini zilitoka bilioni 10.5 tu. Sasa kwa mtindo huu na fedha hizi zilizotoka ni kutoka kwa wafadhili, hata Kambi ya Upinzani imeelezea hilo. Sasa ningependa kujua Serikali wamejipangaje ili tuweze kuwa na fedha zetu wenyewe, ili tuweze kuendeleza maeneo ambayo yanahitajika kuendelezwa? Mfano, kama tunataka kuendeleza Katavi, tunataka kuendeleza kule Southern Circuit, lakini kwa mtindo huu sioni kama wafadhili wakijitoa ina maana hatutaendeleza zile parks nyingine zilizokuwa zinatakiwa kuendelezwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sekta ya utalii ni moja ya sekta ambayo inazalisha ajira nyingi sana. Mfano, Mlima Kilimanjaro kwa mwaka 2017 zilipatikana ajira takriban elfu 20 kwa wapagazi. Hii achilia mbali bado wafanyakazi wa mahotelini, wafanyakazi ambao wanapeleka watu mbugani na kadhalika. Kwa hiyo, ningeiomba Serikali kwa kweli, ihakikishe kwamba, inaichukulia hii sekta very serious.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine cha kusikitisha ni hizi kodi. Tumekuwa tukizungumzia kila siku, unakuta mtu analetewa kodi ya OSHA 1.5 million, kodi ya NEMC 1.5 million, kodi ya COSATA 1.5 million, bado kodi nyingine nyingi tu zaidi ya 36; sasa unajiuliza COSATA wanakuja wanakutoza kwa sababu umeweka television ndani ya hoteli, lakini tukumbuke kwamba, huyu mwenye hoteli bado analipa mfano kwa DStv, Azam Tv na kadhalika. Sasa ningependa kujua OSHA wanakuja wanatoza labda 1.5, wanawasaidiaje hawa wafanyabiashara, hawatoi elimu wanakuja kuangalia kama mmeweka waya vizuri za umeme na kadhalika, lakini return on investment, wanawasaidia nini wale wafanyabiashara ambao wanakuja kuwatoza hizo hela? Hizo hela zinaenda kufanya nini maana hazirudi kwa wale wafanyabiashara kuja kufanya ile biashara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine linalofanya destination ya Tanzania inakuwa expensive ni hizi hidden cost. Unakuta mfano, mtalii akitoka let say Amsterdam kwa package ya siku nane, kutokea kule Amsterdam atalipa dola 4,698 kwa mtu, lakini akija Tanzania analipa dola 5,797 kwa mtu. Kwa hiyo, destination ya Tanzania inaonekana ni expensive sana nami naamini kabisa ni kwa sababu ya hizi tozo ambazo tunaziongeza kwa hiyo, mfanyabiashara kazi yake ni kufanya biashara kwa hiyo, kila chochote anachokipata anakiongezea kwa yule mteja kwa hiyo, destination inakuwa ni very expensive.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningetaka Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara ya Fedha labda watusaidie, high season inakuja mwezi wa Sita na bureau de change wamezifunga. Kwa huu muda mchache walivyozifunga zimeleta bughudha kubwa sana, watalii au wageni wanaokuja kwenye hizi sehemu za wageni unakuta benki zinafungwa saa 10.00 hazi-operate kwa 24 Hours na wakati wa holidays pia zinafungwa na Jumapili zinafungwa, sasa hii inakuwa ni bughudha kwa wageni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nagependa kujua, sidhani kama ni bureau de change zote ambazo zilikuwa zina matatizo, pengine zile zilizokuwa hazina matatizo zingefunguliwa. Kama haiwezekani basi ningeomba Serikali labda walete mobile bureau de change, wawashauri benki wawe na yale magari waweze kutoa hii service kwa sababu hoteli nyingi hawawezi kuweka fedha nyingi ndani ya hoteli kwa sababu ya ujambazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tukiendelea kwa mtindo huu ina maana tunarudi kwenye miaka ya 70 ya black market na watalii au wageni wataanza kutuuzia fedha fake na Tanzania tutakuwa kwenye bad records. Kwa hiyo, naomba twende na wakati, tuko kwenye karne ya 21 jamani, tusirudi tena kwenye miaka 30 iliyopita. Wakati ule tulikuwa tunaficha fedha kwenye vitanda na nini, sasa hivi na sisi twende kwa wakati, sijui hao wanaomshauri Mheshimiwa Rais au walioishauri BOT kufunga zile bureau de change walikuwa wana maana, pengine walikuwa na maana nzuri, lakini sidhani kama kila mtu alikuwa na kosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninalotaka kulizungumzia ni kuhusu utalii wa utamaduni. Nchi zilizoendelea wana-keep historia zao, unatumia majengo kama Ulaya unakuta museam watu wakienda kwenye museam wanalipa fedha, lakini hapa kwetu unakuta kama Dar-es-Salaam tulibomoa majengo yale ya kale na kujenga maghorofa, lakini kuna vivutio vingi sana katika kila wilaya. Mfano mzuri ni kule Moshi Vijijini, Old Moshi, wakati wa Vita ya Kwanza na ya Pili ya Dunia Wajerumani pale Kikarara walijenga mapango kule chini, lakini mapango yale yamekaa tu idle, sasa sijui kama Wizara wanalitambua hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawalitambui basi ni vizuri kwenda kufungua yale mapango iwe kama moja ya vivutio vya utalii ili wale Wajerumani wanavyokuja au tunavyoenda kuuza utalii kule Ujerumani na nini iwe ni mojawapo ya kivutio cha utalii. Kwa ushauri tu, pengine Wizara ingeangalia ni jinsi gani inaweza kutembelea katika kila wilaya wa-identify vitu gani ambavyo vinaweza vikawa ni vivutio na kudumisha utamaduni wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ningependa kuzungumzia kuhusu kuutangaza utalii. Utalii tumekuwa kweli tukiutangaza, lakini mara nyingi wafanyabiashara wamekuwa wakitangaza zaidi na inakuwa ni ghali sana kwao. Sasa nimekuwa nikishauri mara nyingi TTB iwezeshwe ili wafanyabiashara sasa waweze kupunguziwa bei waweze kuitangaza Tanzania zaidi; Mheshimiwa Waziri hapa amesema kuna watalii kutoka Israel walikuja 1,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimjulishe Mheshimiwa Waziri kwamba, hawa watalii waliokuja mwaka huu 1,000 wamekuwa wakija kila mwaka wakati wa low season. Kwa hiyo, asije aka-add up ufikiri labda ni tangazo limefanywa mwaka jana ndio tukapata watalii 1,000. Hawa watalii kutoka Israel 1,000 they have been coming here all these years for the past five years wamekuwa wakija hapa kwa hiyo, sio watu wageni. Inabidi sasa tuangalie ni jinsi gani tunaenda kwenye new destinations huko nchi za Russia, Zchesklovakia na nini, maana sasa hivi ndio utalii mpya umekuja wawawezeshe TTB waweze kwenda kule twende tukaingie kwenye hizi new market sio tung’ang’anie tu hizi market za Ujerumani sijui, Uingereza na Ulaya, lakini twende kwenye hizi nchi ndogondogo nina hakika kabisa tukienda huko tutapata watalii wengi zaidi na tutaongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, nashukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia. Napenda kuipongeza hotuba ya Kambi ya Upinzani; mategemeo yangu Serikali itachukua ushauri uliotolewa na kuufanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hii ya Awamu ya Tano imekuwa ikijigamba ni Serikali ya kutetea wanyonge. Mchango wangu utakua kwa maswali zaidi. Je bajeti hii ni rafiki kwa wanyonge wanaosema wanawatetea? Je itawasaidia kiuchumi? Wanasema uchumi umekua kwa asilimia saba (7%) lakini wananchi huko nje hali ni mbaya sana, uchumi huu umekuwa mwenye makaratasi tu lakini siyo kwa mtu mmoja mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuendelea tunahitaji siasa safi, watu na ardhi. Je siasa za nchi hii ni rafiki kwa maendeleo? Je, sheria zetu ni rafiki kwa maendeleo? Je, bajeti hii imewasaidia sekta binafsi kwa kiasi gani? Je, tozo zilizopungua kwa kiasi gani zinawasaidia wafanyabiashara ambao hawakufunga biashara zao? Je, mfumo wetu wa kodi ni rafiki kwa wafanyabiashara, hawaoni ni wakati muafaka wa kubadili sheria za kodi? Je, mifumo yetu ya benki ni rafiki kwa wafanyabiashara wakati wanakopa sababu riba zipo juu sana 18-22%? Je, mfumo wa masoko kwa wakulima wetu ambao ni zaidi ya 70% ya wananchi ni wakulima Serikali inawasaidiaje kupata masoko? Unakuta mkulima analima mwenyewe, panda, nunua mbegu, mbolea, dawa, anavuna ikifika wakati wa kuyauza mazao yake mfano mahindi inabidi apate kibali kutoka Serikali. Je, Serikali inamwezeshaje mkulima huyu?

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haipo kabisa serious kumsaidia mkulima mfano fedha za maendeleo ambazo zingetumika hata kuzalisha mbegu bora kupata Maafisa Ugani wengi, kuendeleza kilimo cha umwagiliaji wakulima waachane na biashara ya kutegemea lini wingu linajaa uanze kilimo? Bado bajeti kwa ajili ya maendeleo haitoki ya kutosha, mfano mwaka 2018/2019 ziliidhinishwa bilioni 98 lakini zinatoka bilioni 41 tu. Sasa kichekesho mwaka huu 2019/ 2020 wameidhinisha bilioni 143.5, hivi kama mwaka jana hazijatoka mwaka huu zitapatikana wapi? Naomba Waziri anipe jibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tujuavyo magonjwa yasiyoambukiza yanakuja kwa kasi kubwa lakini tunaweza kuyazuia kwa kufanya mazoezi, lakini barabara zetu siyo rafiki kwa watembea kwa miguu, mitaro ya maji taka ipo wazi ni mategemeo yangu kutengwa bajeti ili mitaro ifunikwe na watu wafanye mazoezi kupitia huko na hii itaipunguzia Serikali kutibu watu kwa magonjwa yenye kuweza kukingika sababu na hili Hospitali yetu ya Kanda ya Kaskazini KCMC wamejitahidi na kuanzisha kitengo cha treatment ya Saratani, tayari wamepata machines za kuchoma mionzi lakini vifaa hivi lazima viwekwe kwenye chumba maalum (Banker). Ni vizuri Serikali ikajenga chumba hicho sababu hii itasaidia sana kuondoa msongamano kwenye hospitali ya Ocean Road.

Mheshimiwa Naibu Spika, utalii ni kati ya sekta zinazochangia katika pato la Taifa zaidi ya 17%, lakini bado Serikali haijawekeza ipasavyo katika sekta hii, mfano, tunazo fukwe nyingi, Dar es Salaam, Bagamoyo, Tanga, Mtwara. Je Serikali ina mpago gani na utalii wa fukwe? Mfano Sadan National Park bado hapajawekezwa vizuri, shirikisheni sekta binafsi wajenge hoteli, kuwe na bank, Curio Shop na kadhalika.