Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Salome Wycliffe Makamba (48 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Katiba na Sheria. Pia ningependa kuchukua fursa hii kuipongeza Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwa hotuba nzuri iliyoonesha weledi na uzamifu katika suala zima la Katiba na Sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeeleza yote watu watapiga makofi lakini mwenye macho na masikio atasikia neno hili ambalo watu wa Upinzani tumeeleza Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema inahitaji digrii ya ujinga kukubali kupewa kazi bila job description halafu useme huo ni uamuzi wa bosi wako kama anaweza akakupa au asikupe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuchangia hotuba hii kwa kushauri Serikali mambo yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiwa kama Wabunge kazi yetu kubwa ni kuisimamia na kuishauri Serikali ili iweze kuwatumikia Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutekeleza hayo ningependa kushauri na kuwaomba wanasheria waliopo humu na Mawaziri waliopewa dhamna hii waishauri Serikali itekeleze majukumu hayo kwa kumshauri Rais ipasavyo juu ya utekelezaji wa majukumu hayo kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wafahamu wazi kwamba Urais ni taasisi na siyo mtu binafsi.
Mheshimwa Rais tamko lolote atakalolitoa iwe ni kwa masihara au yupo anakunywa chai au anafanya kitu chochote kwetu sisi tunaiona kama ni agizo na tunaichukulia kama ni sheria, kwa hivyo, Mawaziri wahakikishe kwamba Rais wao anapotoa matamko basi yawe ni ya kujenga na siyo kubomoa Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba suala la uendeshwaji wa nchi hii, tukiangalia suala la sukari, suala la vyombo vya habari, suala la utekelezaji wa haki za binadamu, uendeshwaji wa mahakama ni suala ambalo kimsingi Rais wa nchi hii alipaswa kukalishwa chini na kuelezwa ni lipi aliongee kwenye jamii ambalo mwisho wa siku litaleta matunda na siyo kuibomoa nchi hii na kuirudisha mwaka 1980 enzi za uhujumu uchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, madhara makubwa, leo asubuhi tumepata taarifa kwamba bei ya sukari imefika shilingi 3,200...
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Na hii nayo inasababishwa na tamko ambalo Mheshimiwa Rais alilitoa, tunaamini matamko, sheria, kanuni na taratibu za nchi hii zinafanyika kwa kushirikisha wadau, endapo tatizo au suala la sukari na ukuzaji wa viwanda lingeshirikisha wadau ambao ni watumiaji wa sukari pamoja na wafanyabiashara wa sukari, huenda tusingefikia kwenye hatua hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya mahakama zetu tukubaliane mbali na itikadi zetu za kisiasa ni tatizo ambalo linahitaji kuangaliwa kwa umakini wa hali ya juu. Tunakosa uhuru wa mahakama kwa sababu mahakama hizi kinyume na sheria mbalimbali zilizowekwa ikiwa ni pamoja na sheria za kimahakama na uendeshaji wa nchi hii zimekosa uwezo na uwezeshaji. Nimeshangaa sana Mheshimiwa Mbunge aliyepita aliposema kwamba tusiongelee kwa sababu hii ni mihimili inayojitegemea, lakini sisi kama Wabunge ndiyo tunaopitisha bajeti ambayo inakwenda kuiendesha hiyo mihimili mingine. Kwa hiyo, ni jukumu letu kuhakikisha tunatetea na tunasimamia maslahi ili mihimili hii iweze kuwa independent na iweze kufanya kazi kwa ufanisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mahakama zetu zimekuwa zikikabiliwa na changamoto za miundombinu, malipo ya wafanyakazi na madaraja ya mahakimu; mahakimu wawili wana cheo kimoja, wana daraja moja lakini wanalipwa mishahara tofauti. Suala hili linapaswa kuzungumziwa humu kinyume na mjumbe aliyetoka kuongea anasema kwamba huo ni mhimili unaojitegemea sijui kama yeye ana mfuko wa kuwapelekea mahakama pesa hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Idara ya Mahakama inakabiliwa na changamoto kubwa ya rasilimali. Mwaka wa fedha uliopita Wizara ya Katiba na Sheria ilipangiwa fungu lakini pesa hazikupelekwa ndiyo tunaona inazidi kudorora siku hadi siku. Tumeshuhudia kwenye kesi za uchaguzi, Majaji wanakosa impartiality katika decisions zao, ni kwa sababu ya umaskini wa hali ya juu ulioko katika ngazi ya mahakama. Mahakimu wanapewa baiskeli kwa ajili ya kwenda kazini, wanakosa nyumba, hawawezi kujikimu na hii inapelekea kushindwa kusimamia majukumu yao wakiwa kama mhimili wa Serikali unaojitegemea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijatoka kwenye suala la mahakama mwaka 2012 ulitolewa waraka ambao ulikuwa unaongelea kada ya Mtendaji wa Mahakama. Lengo la kuwa na kada ya Mtendaji wa Mahakama ilikuwa ni kuboresha utendaji kazi wa kiutawala katika ngazi ya Mahakama. Kinyume na mategemeo, kada hii imeshindwa kutekeleza majukumu yake badala yake hali imezidi kuwa mbaya lakini watu hawa wanalipwa na Serikali. Ningeomba Waziri wa Katiba na Sheria aliangalie suala hili kwa umakini sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naomba niongelee suala la Law School. Tanzania tumekuwa na mfumo ambapo mwanafunzi anapomaliza shahada yake ya sheria analazimishwa kwenda kusoma Law School, lakini Law School imekuwa tofauti na shahada ya sheria. Tanzania vyuo vinavyotoa shahada ya sheria viko Mwanza, Mbeya, Arusha na maeneo mbalimbali na Law School ya Tanzania iko Dar es Salaam. Wanafunzi wanalazimishwa kusafiri kutoka huko wanakosomea ambako walichagua mpaka Dar es Salaam kwa ajili ya Law School. Usipofanya hivyo, pamoja na miaka minne aliyoipoteza wakati unasoma shahada yako ya sheria mwanafunzi yule hawezi kutambulika kama ni mwanasheria kamili na hawezi kupata ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na tatizo hilo, wanafunzi hao walio wengi walikuwa wanasomeshwa kwa kutumia mkopo. Cha kusikitisha ni kwamba anapokwenda Law School suala la mkopo inabidi lifanyiwe pre-assessment tena na wanafunzi hawa hawapewi mkopo. Kwa taarifa tu, sasa hivi ada ya Law School ni shilingi milioni moja laki tano na zaidi. Watoto waliokuwa wanasoma shahada ya sheria walikuwa wanalipiwa mkopo na Serikali lakini linapofikia suala la kwenda Law School linakuwa ni jukumu la mzazi kujua yule mtoto atafikiaje kwenye hatua hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili inabidi liangaliwe kwa umakini. Tunayo majengo yako UDOM pale wanakaa buibui, tunayo majengo na watu ambao wanaweza kutekeleza suala hili, lakini leo watu wachache wamejirasimisha zoezi hili wameweka Law School Dar es Salaam. Watu wanalazimishwa kusafiri mpaka Dar es Salaam, hawana makazi, wengine hawajawahi hata siku moja kufika Dar es Salaam, wanalazimishwa wakakae pale wasome Law School kwa sababu kuna maprofesa wachache au watu wachache wanaotaka kunufaika na mfumo huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda suala la Law School lishirikishe wadau hasa wanafunzi wanaokwenda kwenye shule hiyo. Pia ifahamike kuna watu ambao hawakusoma Law School zamani lakini leo kila gazeti utakalolishika linatangaza kazi lazima uwe umepitia Law School. Kwa yule ndugu yangu ambaye hafahamu kiingereza kama alivyoomba afundishwe Law School ni ile shule ya sheria ambayo ni lazima uende kusoma ili uweze kuwa Wakili kwa mujibu wa Law School Act ya mwaka 2007.
MHE. SALOME. W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, namuone huruma sana Mheshimiwa anayesimama na kusema kwamba anakaa Dar es Salaam lakini hajawahi kuona mahakama. Mahakama si kama tangazo la Vodacom au la Tigo linalobandikwa kwenye jukwaa.
MHE. SALOME. W. MAKAMBA: Mahakama ni institution ambayo iko kwa mujibu wa sheria na anachoelezwa ni fact kwa mujibu wa sheria. Unaweza ukakaa Dar es Salaam ukafahamu ratiba ya vigodoro Dar es Salaam nzima lakini usijue ziko mahakama ngapi.
MHE. SALOME. W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Nishati na Madini. Naamini nafasi hii haijaja kwangu kwa bahati mbaya kwa sababu, natokea Mkoa wa Shinyanga ambao umebarikiwa kuwa na baraka ya madini kwa sababu, nina migodi mitatu mikubwa; migodi miwili ya dhahabu, Mgodi wa Bulyanhulu na Buzwagi iliyoko Jimbo la Msalala na Jimbo la Kahama. Nimebarikiwa kuwa na Mgodi wa Williamson Diamonds ulioko Mwadui Shinyanga, lakini pia nina mgodi, medium scale mining wa El-Hilary ulioko Buganika, Kishapu, ukiacha migodi mbalimbali midogo midogo inayohusika na uchimbaji na uchenjuaji dhahabu ambayo imezunguka Mkoa mzima wa Shinyanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Shinyanga ni Mkoa ambao unachangia takribani asilimia tisa ya pato la Taifa hili na hii ni baada tu ya Mkoa wa Dar-es-Salaam na hii inatokana na uwepo wa nishati na madini katika mkoa huo. Pamoja na baraka hizi ambazo Mkoa wangu wa Shinyanga umebarikiwa kuwa nazo leo nikisema niondoke na watu wachache hapa kwenda kuangalia hali halisi ya mkoa huu, ukilinganisha na baraka hizi ambazo tunazo, mambo yanayoendelea kule ni mambo ya kusikitisha sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mkoa wa Shinyanga hasa maeneo ya uchimbaji, walipoletewa habari hii ya uwekezaji wa sekta ya madini walifikiri kwamba, itakuwa ni faraja kubwa kwao na itawakwamua na umaskini, lakini kwa bahati mbaya watu hawa, badala ya mijadala ya kuwahamisha ili kuweza kuwapisha wawekezaji kufanyika kama inavyoelekeza Sheria ya Madini ya mwaka 2002 na 2008 badala yake watu hawa walihamishwa kwa kufukuzwa kama wakimbizi kwenye ardhi yao wenyewe. Mbali na hivyo, watu hawa walilipwa fidia ambayo intervention ya Serikali katika ulipaji wa fidia hizi, ikawa ni kinyume na matarajio ya wakazi hawa, hasa maeneo ya Kakola, ambako kuna mgodi wa Bulyanhulu na maeneo ya Kahama Mjini ambako upo mgodi wa Buzwagi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawa mpaka leo wamekuwa na kilio cha muda mrefu. Zaidi ya miaka 10 wanalalamika kuhusu unfair compensation iliyofanyika kwenye maeneo yale, lakini Serikali ambayo tunaamini kwamba, inaweza kushughulikia matatizo yao haioni umuhimu wa kushughulikia matatizo hayo na wale wananchi wa-feel kweli Serikali ipo kwa ajili ya kuwatumikia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mkoa wa Shinyanga ni wapole na ni watulivu, pamoja na maumivu makali waliyoletewa kwa sababu ya unfair compensation, malipo ya fidia ambayo hawakuridhika nayo, walikubaliana kuvumilia mgodi wakiamini ipo siku Serikali itakuja kutatua matatizo yao. Pamoja na Serikali kutokutatua matatizo yao na kuwaahidi kwamba, watapata kazi kwenye migodi ile, mpaka leo wananchi wale hawapati ajira na wakifanikiwa kupata ajira basi, watapewa zile ajira ambazo mwisho wa siku zitawaacha katika hali ya umaskini mkubwa na utegemezi wa hali ya juu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wanaozunguka eneo la mgodi wakipata kazi kubwa katika migodi hii ambayo tunaamini ni ya wawekezaji watapata kazi ya kufagia, kufyeka, upishi na hakuna program zozote za msingi ambazo ni madhubuti zimewekwa na Serikali zinazoweza kuwaendeleza wananchi wale! Japokuwa tunasema wamefanya kazi kwa muda mrefu tuna-assume kwamba, wana-on job training, basi angalau i-certify ujuzi walionao ili siku moja watu wale waweze kuja kupata kazi ambazo zitawaingizia kipato na cha akiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisikitishwa sana na matukio yaliyojitokeza kwenye Mgodi wa Bulyanhulu miaka ya 2000, 2002, 2005; wafanyakazi wale walipata ulemavu, wengi wao wakiwa ni ma-operator. Wale ambao tulipata bahati ya kwenda kutembelea migodini kuna Watanzania wenzetu wanaofanya kazi ya ku-operate mitambo katika migodi ile, lakini pamoja na maradhi waliyoyapata kwa sababu ya kufanya kazi ngumu na nyingine zikiwa underground, watu wale walipelekwa kutibiwa na mgodi na wakiwa wanaendelea na matibabu yale, wale watu walirudishwa kazini na kufukuzwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi zao ziko Mahakamani. Mpaka leo wanahangaika wengine wanakufa kwa sababu ya magonjwa, lakini Serikali inayojiita Serikali sikivu, sijaona hatua mahususi, hatua madhubuti za kusaidia kutetea watu hawa na leo hii tunajisifu hii ni Serikali ya Hapa Kazi Tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha mbali suala la watu kufukuzwa kazi, kuna watu ambao leo migodi ya Tanzania, migodi ya wawekezaji imekuwa ni Serikali ndani ya Serikali ya Tanzania. Wafanyakazi wanapokosea katika migodi ile adhabu wanayopewa bila kujalisha ukubwa wa kosa alilolifanya anapewa adhabu ya kufukuzwa kazi na anafungiwa haruhusiwi kufanya kazi mahali popote pale maisha yake yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala limewaathiri watu wengi ambao kama nilivyotoka kusema awali, wananchi wa Mkoa wa Shinyanga maisha yao yote yamekuwa ni maisha ya madini. Unapomwambia kwamba, haruhusiwi kufanya kazi tena ina maana unamzuia yule mtu kupata kipato halali na hakuna adhabu Tanzania hii, labda kama ni adhabu ya kifo, inayomfanya mtu kupewa adhabu ya milele, lakini hicho ndiyo kinachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo migodi inafungwa! Tumeona Mgodi wa Tulawaka umefungwa na Mgodi wa Buzwagi huenda mwakani ukaanza closure plan na migodi mingine itafungwa. Kinachotokea nyumba zinazozunguka migodi hii zimekuwa zikipata athari kubwa ya uwepo wa migodi hiyo, kama athari za milipuko na athari za kemikali inayoweza kuvuja kutoka migodini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini leo Tulawaka imeshafungwa na Buzwagi itafungwa. Vijiji vya Mwendakulima, Vitongoji vya Ikandilo, Chapulwa, Mwime, Mbulu, Kakola, kule Msalala watu wanalia, nyumba zao zimepata crack, zimepasuka kwa sababu ya athari ya milipuko! Nimewahi kushiriki kwenye Kamati kwa ajili ya kuangalia athari za milipuko na Kamati hizi zilishirikisha watendaji wa Serikali ambao ni Majiolojia na Maafisa Madini. Afisa Madini anakuja kwenye Kamati ya Uchunguzi wa Athari ya Milipuko na kalamu na karatasi; utawezaje kuchunguza athari ya mlipuko kwenye nyumba bila kuwa na vifaa ambavyo vinaweza kukupa data zinazoeleweka Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea ku-improve sekta ya madini na uwekezaji, tunaongelea kuwapa vifaa Wataalam wa Serikali ili tuweze kupata ripoti ambazo zipo impartially, ambazo zinaweza kusaidia na kutetea maslahi ya wafanyakazi wetu na wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda Nyamongo kuna kesi, hata leo ukifungua kwenye google, kuna kesi inaitwa the Tigiti River; ile kesi watu waliripoti, Wabunge walipiga kelele Bungeni na mto ule ulikuwa unatiririsha maji yanayotoka mgodini ambayo yalisemekana kwamba yana sumu, yalitiririshwa kwenda kwenye vijiji na ng‟ombe wakafa na watu wakaathirika, lakini Serikali ikapuuza kelele za Wabunge, kama ambavyo mnafanya sasa! Matokeo yake ripoti ya Umoja wa Mataifa na Mataifa mbalimbali ndiyo iliyofanyiwa kazi. Hivyo, leo tutaendelea kupiga kelele humu ndani na kama kawaida Serikali itapuuza, lakini naamini sisi tukiongea msipofuatisha na mawe yataongea na ipo siku mtatekeleza matakwa ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nielekee kwenye suala la uchimbaji holela. Katika Wilaya ya Bukombe kuna Pori la Kigosi Moyowosi na Sheria ya Wanyamapori ya Mwaka 2009 inasema, hairuhusiwi kuchimba madini hasa ya dhahabu except for strategic minerals. Lakini leo…
MWENYEKITI: Ahsante, muda wetu ndiyo huo!
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Mpango huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa namsikiliza kwa makini sana Mheshimiwa Waziri wakati anawasilisha Mpango wake na nikazidi kupata maswali mengi ya utekelezaji wa Mpango wake kwa sababu mambo mengi ambayo ameyaandika yanaonekana kwenye nadharia na huenda yasitekelezwe au yasitokee kabisa kama Mpango uliopita. Mheshimiwa Waziri anasema kwamba anataka kuweka mazingira mazuri ya kibiashara kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunafanya maendeleo ya viwanda Tanzania
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mazingira hayo mazuri ya kibiashara Mheshimiwa Waziri hakuyaeleza kinaga ubaga na hilo linanitia mashaka, kwa sababu nikifikiria moja kati ya vitu ambavyo ni vya kipaumbele ili tuweze kukuza viwanda Tanzania tunaongelea habari ya umeme, miundombinu lakini mpaka leo na hata ukiangalia katika bajeti tuliyonayo hakuna nguvu ya ziada ambayo Serikali imeiweka kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapata maendeleo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano wa mazingira ambayo tunaishi Watanzania leo, bei ya umeme bado iko juu na wanasema kwamba wamepunguza kwa asilimia mbili lakini effect yake katika punguzo hilo haionekani katika uhalisia wa maisha ya Mtanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia katika mazingira ya sheria ambazo Mheshimiwa Waziri alitakiwa azieleze kwamba ndiyo zimerahisisha utekelezaji wa sera hii ya viwanda, sioni kama ameonesha kwa njia yeyote ila ameweka sheria kwa ajili ya kuvutia wawekezaji wadogo wadogo, labda kama yeye alipokuwa anaongelea maendeleo ya viwanda alikuwa anaongelea wawekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii wawekezaji wadogowadogo hasa wale wanaohusika na mazao ya kilimo wanawekewa vikwazo, wanawekewa sheria ngumu na wanawekewa tozo mbalimbali ambazo mwisho wa siku zinawafanya wazidi kukwama katika harakati hii ya kujiendeleza katika kutengeneza malighafi kwa ajili ya maendeleo ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano moja katika Jimbo la Kahama Mjini, Jimbo lile kuna watu wanashughulika na biashara ya upakiaji na uchakataji wa zao la mpunga, lakini leo hii ukiangalia tozo ambazo wanatozwa watu wale mpaka wanafikia hatua ya kukata tamaa kujihusisha na zao hili la kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wamewekeza fedha zao kwa ajili ya kutengeneza na kupaki zao hili la mpunga, lakini kuanzia asubuhi mpaka jioni umeme hauwaki, ukiwaka jioni Polisi wanapita wanasema hairusiwi mtu kufungua kiwanda usiku. Kwa hiyo, wanajikuta ndani ya mwezi mzima watu wale wanashindwa kufanya uzalishaji, kwa hivyo hata zile fedha ambazo wamewekeza mle wanashindwa kuzirejesha kama walizikopa kwenye mabenki, lakini pia wanashindwa kuzizalisha ili ziweze kuwaletea faida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawa ukiangalia ambao ni wazalishaji, Mheshimiwa Waziri anasema kwamba, anataka kuendeleza viwanda, lakini nimesikitishwa na taarifa ya Waziri anasema kwamba bei za mazao zinapaswa zizidi kushuka. Swali hasa lilikuwa limeelekezwa kwenye zao la maziwa ambapo Mkoa wa Shinyanga tunafuga sana ng‟ombe, kwa sasa hivi lita ya maziwa ni shilingi mia nne mpaka shilingi mia tano na watu wale hawanufaiki, kumfuga yule ng‟ombe ni gharama, sindano moja inakugharimu kuanzia laki nne mpaka tano kwa ngombe mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ile shilingi mia nne, shilingi mia tano kwa lita ya maziwa unaambiwa izidi kushuka sasa sijui yauzwe lita moja shilingi mia mbili, hapo sijamuelewa vizuri! Kwa maana hiyo, ni kwamba, tunawakatisha tamaa wakulima, tushushe bei ya zao la maziwa, tushushe bei ya zao la pamba, tushushe bei ya zao la tumbaku, halafu unasema watu tuko katika harakati za kuzalisha malighafi ya kutosha ili tuweze kuendeleza viwanda Tanzania!
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisikia kauli mbalimbali za Serikali zikibeza misaada, lakini ukiangalia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri inasema wazi kwamba gharama kwa ajili Mpango huu wa Maendeleo itakuwa ni trilioni 107 na Serikali itatoa trilioni 59 tu, hiyo baki inayobaki tunategemea kuitoa wapi? Bila shaka fedha hizo huenda zingetoka kwa wahisani au wafadhili na labda kukopa kwenye mabenki ambapo mwisho wa siku inaonekana kwamba fedha hizo tunashindwa kuzirejesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshindwa kutoa kauli badala yake inazidi kuwabeza hawa watu. Sasa hivi tuko katika ulimwengu wa teknolojia, wanazipata hizi taarifa na hakuna mtu yeyote anayeshtuka na kuona kwamba yule mtu anayetusaidia angalau kidogo tunatakiwa tumheshimu, badala yake tunatoa kauli za kukejeli na kauli za dharau, wakati leo hii waziri anathibitisha wazi kwamba ana zaidi ya nusu ya gharama ya bajeti ambayo hajui atakapoitoa. Matokeo yake anategemea kwenda kuzidi kuwabana watu kwa kuchukua property tax za Halmashauri, anategemea kwenda kuwabana watu kwa kuchukua kodi mbalimbali ambazo Halmashauri inakusanya kwa ajili ya kujiendesha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia katika mazao mbalimbali ambayo leo hii yalitegemewa yatunufaishe Watanzania. Wakati tunachambua sheria ndogo za Halmashauri, tulionamkulima amebebeshwa mzigo mkubwa sana. Kwa mfano, moja kati ya sheria ndogo mkulima anaambiwa achangie mpaka fedha kwa ajili ya Mwenge, hivi kweli Mwenge, kwa nini Serikali Kuu isitoe hiyo pesa kama kweli inaona hilo jambo ni la muhimu sana hata inambebesha mkulima mdogo kutoa hiyo pesa ikiwa ni moja kati ya tozo ambayo imelimbikizwa katika zao lake lile ambalo anategemea kuzalisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sioni sehemu ambayo Mheshimiwa Waziri ananieleza juu ya kuboresha ufundi stadi ili kuweza kupata watu ambao wataweza kufanya kazi katika hivi viwanda ambavyo vinategemewa kuanzishwa. Katika mikoa tumeona kuna VETA moja tu katika kila Mkoa na mtu anavyotaka kufungua Chuo cha Ufundi Wilayani kuna ukiritimba mwingi na process ndefu ambayo inamkwamisha mtu binafsi kuweza kufungua Chuo cha Ufundi au Chuo cha VETA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri afahamu kabisa kwamba tunayo sera ya kwamba mwekezaji anatakiwa kuajiri watu wanaozunguka eneo alilowekeza. Walio wengi na miradi mingi inawekezwa maeneo ya vijijini na maeneo yale hayana watu ambao wana elimu ya juu na wanategemea kupata watu ambao angalau wanaweza kuwa na elimu ya ufundi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano wa mgodi wa Buzwagi na Bulyanhulu ambayo ipo katika Vijiji vya Kakola na Wilaya ya Kahama, maeneo yale watu wengi siyo kwamba wana elimu ya juu, lakini hakuna Chuo cha Ufundi kwa ajili ya kuendeleza wale watu, unamkuta mtu anafanya kazi ya kibarua zaidi ya miaka minne, mitano, kwa sababu hana jinsi ya kusoma angalau masomo ya jioni ili aweze kupanda kutoka ile rank aliyopo kwenda juu, inambidi aendelee kufanya kazi ile itakayomtesa kwa miaka nenda miaka rudi halafu leo Waziri anasema anataka kuendeleza ufundi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado sijaelewa vizuri mkakati wa Waziri anaposema anataka kuuza viwanda, kwa sababu kwa upeo nilionao ni kuwa viwanda vikubwa vinatokana na viwanda vidogovidogo ambavyo vinaanzishwa na wananchi wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii pale Kahama tunalo soko la wakulima, wale watu wamejiunga kwenye ushirika na wamekusanya fedha zao wamejitahidi wameweza kutengeneza lile soko na leo linaonekana ni moja kati ya masoko makubwa katika Mji ule. Hata hivyo, leo ukiangalia soko lile Serikali imekubali ule ushirika kuupeleka ukauzwa kwa mtu binafsi, wakati Sheria ya Ushirika iko wazi kwamba soko lile lilitakiwa liuzwe kwa ushirika mwingine ulio hai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili linaungwa mkono na Serikali, kibali kimeshatoka, soko lile ambalo wananchi wamekusanya jasho lao linapelekwa kupewa mtu binafsi, wakati wale watu waliweka nguvu. Nilitegemea Serikali iwasaidie, iwawezeshe, iwape mtaji ili lile soko liweze kuwa kubwa, liweze kukidhi mahitaji ya ndani na ya nje ya Mji ule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutilia mkazo katika elimu. Kama kweli tunataka kwenda katika biashara ya viwanda ni lazima tuhakikishe tunatoa elimu ambayo ni ya ubunifu na wananchi wana uwezo wa kutoa ubunifu kwa ajili ya maendeleo ya viwanda. Elimu tuliyonayo leo hii ni ile ya kukariri, ndiyo maana unasikia mara leo Mama Mheshimiwa Ndalichako anasema kuna GPA, mara anarudi kwenye Division, ni kwa sababu hatuna system ambayo inaweza kutambua njia sahihi ya utoaji wa elimu Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tuko serious hatuwezi kusema tunaenda kuendesha elimu kwa njia ya mtu kutoa matamko tu kwenye magazeti. Elimu inatakiwa iboreshwe kwa kufanyiwa utafiti na ikidhi mahitaji ya Watanzania na siyo kwa kukidhi mahitaji ya Serikali ya CCM inasema hivi, kesho inakuja Serikali nyingine inasema mnawayumbisha watoto mnawa- frustrate, naomba Serikali iwe serious tunapoongelea masuala ya elimu kwa ajili ya mabadiliko ya viwanda hatuongelei tu suala la kufurahisha chama fulani au chama fulani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, ningependa kuongelea suala zima la miundombinu. Barabara za Mitaa na barabara za TANROAD, barabara hizi zimegeuzwa kama mitaji. Tunayo barabara ambayo inatoka Kahama inaelekea Kakola pale Jimbo la Shinyanga kuunganisha na Jimbo la Msalala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inafahamika wazi kwamba uwezo wa ile barabara haiwezi kubeba magari ya ukubwa wa namna ile ambayo yanapeleka mizigo mbalimbali kuelekea mgodini na kuelekea Geita, badala yake TANROAD imegeuza ile barabara kama mtaji, kila mwaka ile barabara inafanyiwa repair, inamwagiwa kifusi na ku-level, sasa hivi ni zaidi ya miaka kumi tangu mgodi ule umeanzishwa barabara ile inafanyiwa repair kila mwaka na mamilioni ya fedha yanapotea. Naomba Waziri husika alitazame hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea maendeleo ya viwanda hatumaanishi kudunduliza pesa, bora kama fedha ni ndogo basi tuwekeze mahali ambapo tunaona kwamba italeta tija na italeta maendeleo ya nchi hii, lakini siyo tunaruhusu watu wanatumia hii kama ni njia ya kujinufaisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa mchango wangu kwa maandishi ili na mimi niweze kushauri Serikali katika kuboresha sekta hii muhimu ya elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Wizara ya Elimu itoe fursa kwa watu binafsi wenye uwezo kuwekeza katika elimu ya ufundi VETA. Hii itasaidia kuipunguzia mzigo Serikali unaotokana na ufinyu wa bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mimba za wanafunzi, Wizara ilete Muswada Bungeni utakaoonesha jinsi ya kuwabana na kuwawajibisha wale wanaohusika na mimba hizo. Pia Serikali iweke mtaala maalum kwa wasichana wanaozalia shuleni ili tusije wapa haki ya kusoma na kujikuta tunakandamiza haki ya watoto waliozaliwa mfano haki ya kunyonya, kuwa karibu na wazazi lakini pia tusijeleta mzigo mkubwa wa kulea kwa bibi watakaokuwa wakilea watoto hao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tujitahidi kutoa motisha kwa Walimu ili kuwapa morali katika utendaji kazi wao. Natoa mifano michache ya baadhi ya Walimu niliokutana nao katika Wilaya ya Kyerwa kwenye moja ya ziara zangu. Walimu hawa walipandishwa vyeo miaka miwili iliyopita lakini mpaka leo hawajaongezewa mishahara. Nafahamu changamoto ya bajeti inayoikabili Serikali yetu ila nashauri tusiwapelekee barua za kuwapandisha vyeo kama hatuna uhakika na malipo yao. Baadhi ya Walimu hao ni kama ifuatavyo:-
(1) Rutaihwa Kazoba
(2) Geofrey Kamondo
(3) Rugeiyamu Damian
(4) Selestine Tibanyendera Ishengoma
(5) Erick Twesige Anacleth
(6) Philbert Jeremiah Kazoba
(7) Tabu Herman
(8) Ndyamukama Cylidion
(9) Heavenlight Baguma
(10) Frida Buyoga
(11) Onesmo Alphonce
(12) Philbert Kinyamaishwa
(13) Diomedes Kajungu
(14) Yohatam Samwel
(15) Diomedes Kajungu
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema awali hao ni baadhi ya Walimu waliopo katika Wilaya ya Kyerwa ambao nilipofanya ziara yangu ya kiutendaji niligundua hao na wengine wengi ambao majina yao sijayataja wamepandishwa vyeo kwa takribani miaka miwili sasa na mpaka leo hawajaongezwa mishahara. Naomba Mheshimiwa Waziri ufuatilie matatizo haya katika Wilaya ya Kyerwa na upatapo nafasi naomba unijibu hoja zangu hizi kwa maandishi ili niweze kupeleka mrejesho kwao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, napenda kumwomba Waziri ashirikiane na Wizara ya TAMISEMI ili kuweza kusukuma vipaumbele ambavyo kimsingi Wizara hii mnakutana navyo moja kwa moja katika kutekeleza Sera ya Elimu nchini. Nakutakia kila la kheri katika kutekeleza majukumu yako, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekaa najiuliza swali moja, hivi hii Serikali ya Awamu ya Tano ndiyo Tanzania ya Viwanda au ilikuwa ni Serikali ya Awamu ya Nne? Kwa sababu kinachofanyika sasa hivi, mwaka 2014/2015 katika bajeti ambayo Waheshimiwa Wabunge wenzetu walikuwepo humu waliipitisha, asilimia 82 ya bajeti ilipelekwa kwenye viwanda na vikaboreshwa. Leo 2015/2016 bajeti ya shilingi bilioni 35.3 tumepeleka shilingi bilioni 1.6 sawa na asilimia 5. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha hiyo, mwaka 2016/ 2017 tumepeleka 8% ya bajeti nzima. Mwaka 2018 mpaka Machi, taarifa tuliyopewa kwenye Kamati tumepeleka asilimia 9.4 tu yaani hakuna mwaka ambao tumepeleka angalau asilimia 50 ya bajeti ya viwanda halafu tunajinasibu kwamba tunaenda kwenye Serikali ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala linanipa wasiwasi na ndiyo maana ukiona mtu anajitetea sana, ujue kuna maovu nyuma yake. Ndiyo maana ukiangalia viongozi mbalimbali wa Serikali wana matamko tofauti tofauti juu ya ni viwanda vingapi vimeanzishwa Tanzania mpaka leo hii?

Mkuu wa nchi anasema tumeanzisha viwanda zaidi ya 3,060, Waziri kwenye hotuba yake anasema kwamba ameanzisha viwanda 1,287, kitabu cha Mapendekezo ya Mpango wanasema viwanda viko 50. Kila mtu anaongea statement yake, Serikali moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima ujichanganye kwa sababu Watanzania tumewaaminisha tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda. Laiti kama Watanzania wangegundua kwamba viwanda wanavyoahidiwa kwenye kampeni ni vya kutengeza juisi, zile blender, ni viwanda vya cherehani, sijui kama leo tungekuwa tunaongea haya maneno. Leo tumebadilishiliwa story tunaambia kwamba viwanda ni aina yoyote, vya kati na vidogo. Sawa, basi hivyo viwanda vidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma kwenye ripoti ya CAG, SIDO wanaweza kutoa mikopo kwa asilimia 40 tu ya pesa ambazo walikuwa wame-propose kwamba wanatoa mikopo. Watu wanaoahidiwa watapewa mikopo kwa SIDO ndio hao wenye viwanda vya kati na viwanda vidogo lakini pesa hawapelekewi. Mheshimiwa Waziri anajitapa hapa ameanzisha viwanda vipya. Jamani, wengi hapa sisi ni wazazi. Hivi kweli mtoto wako hata kama una watoto wengi kiasi gani, mtoto wako mmoja akifa kwa kifo ambacho umesababisha wewe mwenyewe mzazi utajisikiaje? Viwanda vinakufa vidogo na vya kati, pesa hatupeleki halafu tunajinasibu kwamba tunatengeneza Serikali ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika bajeti ya mwaka 2018, hiyo 8% ninayosema imepelekwa siyo fedha za ndani, ni fedha za wafadhili, fedha ambazo tunapewa na watu wengine. Uangalie seriousness ya Serikali katika kukuza uchumi wa viwanda, wewe mwenyewe utaona kuna changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme, ili viwanda viweze kukua, Mheshimiwa Waziri atakubaliana nami kwamba lazima tukuze malighafi, lazima tuhakikishe tunaboresha pamba, tumbaku na barabara. Shinyanga ni wakulima wakubwa wa pamba. Sisi mpaka sasa hivi tuna- export pamba tani 700,000. Yes, tunauza marobota 700,000 lakini tuna-import marobota ya nguo 2,000,000 kuleta Tanzania. Mbona tunafanya biashara kichaa? Kwa nini Serikali isiwekeze kwenye malighafi ili kukuza viwanda?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namweleza Mheshimiwa Waziri, hivyo viwanda anavyovitaja kwenye kitabu chake wanampigia makofi, anapiga nao picha, anatuma kwenye mitandao, hao watu wanamwangalia waone yeye ana commitment gani kukuza viwanda? Wale watu wamewekeza Tanzania lakini Waziri unathubutu kukaa na Wizara ya Uchukuzi, Wizara ya Miundombinu na Wizara ya Kilimo kuangalia utarahisisha vipi uzalishaji kwenye hivi viwanda? Au tunafanya majaribio ya kusema tumeleta viwanda na baada ya miaka mitano viwanda vimeshindwa kufanya kazi au viwanda vyote vimefungwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi viwanda anavyotuaminisha leo Mheshimiwa Waziri, hebu jiulize swali, vinaajiri Watanzania wangapi? Juzi nimesikia Mheshimiwa Waziri anasema kwamba cherehani tano ni kiwanda. Mheshimiwa Waziri tusifanye mchezo na Watanzania, wanatutegemea sisi Wabunge na Serikali kuamua hatima ya maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda kwangu Kahama, Shinyanga na Mikoa ambayo kimsingi ilikuwa imekaa strategic kibiashara, nikikueleza tangu Serikali yenu imeingia madarakani, zaidi ya asilimia 70 ya wafanyabiashara waliokuwa wanamiliki maduka na biashara wameshapokonywa mali zao na Serikali. Watu wana mikopo Mheshimiwa Waziri. Wewe unachekelea kuleta viwanda vipya, una mkakati gani kuhakikisha viwanda ambavyo vilikuwepo ambavyo kimsingi vilikuwa vinalipa kodi na vinaendesha Serikali unavi-maintain? Una mkakati gani wa kuhakikisha hawa watu pamoja na kutusaidia kuendesha Serikali, wanaendelea kuwepo kwenye circular ya uchumi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa nakaa namfikiria Mheshimiwa Waziri, sijui anaposema kwamba tuna viwanda 3,000 anakuwa ana-project nini? Kwa sababu kama mwisho wa siku Shinyanga pale kuna Kiwanda cha Nyama hakina uwezo wa kuajiri hata watu 2,000. Shinyanga leo maji na barabara ni changamoto, ng’ombe ndiyo kwanza mmekazana kupiga chapa mnakusanya ushuru wa Sh.5,000, umeme ndiyo kabisa, labda wanunue na power bank pale kwenye kile kiwanda, hali ni mbaya, lakini Mheshimiwa Waziri anajinasibu anasema viwanda vinaendelea, tunafanya vizuri, tunafanya vizuri wapi? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka commitment ya Serikali, tutafanyaje kuhakikisha wawekezaji wa kati na wadogo ambao ni wafanyabiashara kwa Tanzania hii na ndiyo walezi wa Tanzania hii, wanarudi kwenye hali yao ya kiuchumi kuweza kuendesha nchi hii? Nataka commitment ya Serikali juu ya huu utaratibu wenu, mtu akiamka asubuhi, TRA inapanga leo tunatoza kodi kiasi hiki, kesho asubuhi wanasema kiasi hiki, nini commitment ya Serikali? Watu wanafunga biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa leo, huyo huyo ambaye ni sehemu ya Serikali, anasema mnaofunga maduka, fungueni, njooni mezani tuzungumze, tunaweza tuka-negotiate bei ya kulipa kodi TRA.

TAARIFA . . .

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri, halafu naomba kitu kimoja, tukiwa tunawashauri muwe mnatusikiliza kwa sababu Tanzania nzima haiwezi kuja hapa kuongea, sisi ni Wawakilishi wa wananchi. Tena kwa taarifa yako, kule kijijini njoo kwangu watu wanapiga chapa ng’ombe mpaka Sh.7,000 siyo Sh.5,000, ninyi mmekaa hapa sisi tunatoka kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuhusu suala la kiwanda, mimi kwa uelewa wangu, kwa mujibu wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania, anapokuja kuwekeza Tanzania anapewa kitu kina tax incentive. Akipewa incentive, maana yake kwa kipindi cha muda fulani yule mwekezaji hatalipa kodi mpaka ambapo ule muda wa incentive uwe umeisha. Kama hiyo haitoshi, kuna kitu kinaitwa operational cost, yule mwekezaji yuko pale hana miaka miwili, amekuwa anafanya operation pale na halipi kodi kwa sababu anasema costs zake za uzalishaji hazijalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Serikali wanatujia hapa na mazingaombwe eti wanatafuta mbia mpya, what about the incentive? Vipi kuhusu ile tax holiday mliowapa wale wawekezaji? Jamani nyie si mnajisema kwamba ninyi ni Wataalam, ni wataalam wa nini basi? Tusifanye siasa kwenye maisha ya Watanzania. Siasa hizi zitakuja kutuadhibu, makaburi yetu yatapigwa fimbo na wajukuu zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusijifiche nyuma kwa kusema kwamba Serikali inatafuta mbia. Mheshimiwa Waziri hata standard gauge miujiza hii hii ilifanyika. Tumeacha mkopo wenye riba ya asilimia 1.2 tumeenda kuchukua mkopo wenye asilimia 4. Unakaa unasema umekaa na wataalam wanakokotoa mimi sijui mahesabu au biashara, lakini kwa uelewa wangu tu wa kawaida, siwezi kufanya biashara ya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali iwasaidie Watanzania, itengeneze miradi. Wakae pamoja, naamini Balaza la Mawaziri ni moja, wamsaidie Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara tutengeneze miundombinu kwa ajili kusafirisha malighafi na tuboreshe zao la pamba. Zaidi ya Watanzania milioni 16 wa Lake Zone wanalima pamba. Mheshimiwa Rais anasema hao ndiyo wapiga kura wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kilimo chetu tunategemea pamba. Hebu tuboreshe zao la pamba ili tuweze kufungua viwanda vya nguo na kufungua viwanda vya mafuta. Leo kelele za mafuta zisingekuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikitembea tu kidogo kilometa moja kutoka nyumbani, naona maua ya pamba yametanda kila mahali, leo tuko busy tunanunua ndege, tunajenga flyover, Tanzania siyo Dar es Salaam, Tanzania ina Mikoa zaidi ya ishirini na kitu. Tanzania siyo Dar es Salaam.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 7) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa dakika mbili japo ni chache nitajitahidi. Nilitaka kuongelea mambo makubwa mawili, jambo la kwanza ni kuhusu Tume ya Marekebisho ya Sheria. Tumekuwa tunaona sheria nyingi zinaletwa ndani ya Bunge kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho tangu 2015 nimeingia hapa Bungeni na marekebisho hayo yana lengo la kuongeza Vifungu vya faini au kifungu, yaliyo mengi. Jambo ambalo kiukweli ninaona sheria karibu zote zimeshapitwa na wakati kwenye Vifungu vya faini na kifungo. Zipo sheria zinasema mpaka mtu atatozwa faini shilingi mia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Tume ya Mabadiliko ya Sheria wanafanya nini pale ofisini? Kwa nini wasifanye marekebisho ya sheria? Sheria ya Role Visions Act inataka marekebisho ya sheria yafanyike kila baada ya miaka kumi. Marekebisho ya kwanza yalifanyika mwaka 1966, ya pili tumefanya 2002, miaka 36 baadaye. Nimuombe Attorney General asiendelee kutumia rasilimali za watanzania kuleta marekebisho madogo madogo, liko tatizo la msingi iitwe Tume ifanye mabadiliko ya sheria zote ili ziendane na wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nilitaka kuzungumza, ni kuhusu hili la kufifilisha kosa. Bado naendelea kung’ang’ania pale kwamba kama mtu amekiri, kosa limefifilishwa, yule mtu ameshindwa kulipa, ninaamini ziko.., Mheshimiwa AG nakuomba unisikilize tafadhali. Kama kosa limefifilishwa, mtu ameshindwa kulipa ziko sababu nyingi hasa kwa mazingira ya sasa ya mtu kushindwa kulipa fedha au faini ambayo kosa lake limefifilishwa. Kwa mantiki hiyo…
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 6) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kwa dakika hizi chache nami niweze kutoa mchango wangu katika mabadiliko haya Na. 6 ya sheria yaliyoletwa kwenye Bunge letu Tukufu.

Mheshimiwa Spika, mimi yangu leo ni mawili ambayo ningependa kufafanua baada ya hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani. Napenda kushauri Serikali katika mabadiliko aliyoyaleta katika Sheria ya EWURA Kifungu cha 6 wafute Kifungu cha 3 ambacho kinasema kwamba mtu anaposhindwa kulipa deni la kosa ambalo limefifilishwa, basi Mamlaka, yaani Mamlaka ya EWURA ina huwezo wa kumtoza riba.

Mheshimiwa Spika, lengo la kufifilisha kosa na wameeleza vizuri kwenye madhumuni ya Muswada huu kwamba wanafifilisha kwanza ni kuokoa muda wa kupeleka kesi Mahakamani lakini pili ni kuruhusu biashara ziweze kuendelea. Mtu huyu ameshakiri kwamba ni kweli amefanya kosa na akakubaliwa kulipa nusu ya deni ambalo angeweza kulilipa akienda Mahakamani, sasa katika mazingira ya kawaida ya kibiashara tuseme EWURA ina-deal na wanaomiliki vituo vya mafuta na maeneo ya namna hiyo. Kama ameshindwa kulipa deni na hajakataa kulipa, ukimtoza riba tafsiri yake unamwongezea kwenye deni lile la msingi.

Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo tunafahamu wote mazingira ya kibashara Tanzania yalivyo sasa hivi, wakati mwingine biashara haziendi vizuri, wakati mwingine mtu anakwama kwa sababu watu wanaohusika na biashara zinazohusiana na EWURA wengi wana mikopo benki, kwa hiyo, wakati mwingine mtu anaweza kushindwa kulipa kwa sababu ya kibiashara. Kumtoza riba mtu huyu ni kumwongezea mzigo juu ya mzigo ambao tayari amekiri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali isimtoze riba mtu ambaye amekiri kosa lake, amekubali kulipa, lakini ameshindwa kulipa. Badala yake wanazo nafasi mbili za kufanya; kwanza, wanaweza kukaa mezani na kuzungumza naye namna bora ya kumsaidia aweze kulipa deni hilo. Hii alifanya Mheshimiwa Dkt. Mpango wakati wa wasilisho lake la Wizara ya Fedha kwenye Bajeti iliyopita, akawaongezea muda watu ambao walikuwa wanadaiwa madeni ya kikodi na TRA na ambao walikubali. Kwa nini tusifanye hivyo kwa watu ambao makosa yamefifilishwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali ili kuonesha kwamba wao sio washitaki, sio waamuzi na wao ndio kila kitu, wanaweza kupeleka jambo hili Mahakamani kama inavyoelezwa kwenye Kifungu kidogo cha (4) kilicholetwa kwenye marekebisho ya Mswada bila kumtoza riba mfanyabiashara huyu. Kwa hiyo, kama ameshindwa kulipa na Serikali wameshindwa kuafikiana, basi kesi hiyo ipelekwe Mahakamani ikaamuliwe Mahakamani na mtu yule aweze kulipa kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo niongeze pia katika kifungu kinachohusiana na vifuko vya feri. Katika mabadiliko clause No. 18 ya Muswada huu wa Marekebisho, wanasema kwamba kwenye Kifungu kidogo cha (3), mtu yeyote atakayeingilia shughuli za kivuko, shughuli zozote zile; atakayefanya shughuli ambazo zitaingilia kivuko, basi atatakiwa kulipa faini ya shilingi 50,000/= mpaka shilingi milioni 10 nimeona kwenye mabadiliko ya Serikali au kufungwa miezi sita au vyovyote kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa jumla sana kwenye kifungu hiki na tuliwashauri vizuri sana kwenye Kamati, waeleze hizo shughuli za binadamu wanazosema zitaingilia kivuko ni zipi? Kwa sababu nimesoma vizuri kwenye hotuba yetu kwamba unaposema shughuli za kibinadamu zitakazoingilia shughuli za kivuko, zipo tofauti na zinatofautiana kwa madhara. Leo huwezi kusema unamtoza mtu aliyeingilia shughuli za kivuko, kwa mfano, pale kwenye kivuko cha Kigamboni Dar es Salaam, kwa sababu ameogelea, basi unamtoza shilingi milioni 10 kwa mfano, kwa sababu kiwango cha ukomo ni shilingi milioni 10. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine kuna watu kweli nakubali wanafanya makosa makubwa kama uvuvi wa kutumia nyavu ambao unaweza ukaharibu kabisa feri yetu. Kwa hiyo, niseme, moja kati ya jambo ambalo linawapa wakati mgumu watafsiri wa sheria kwa maana ya Mahakama ni kuelewa dhamira ya Bunge. Nasema hayo kwa sababu sisi leo tutapita, hii sheria inabaki inaishi, tutawapa changamoto kubwa watakaokuja mbele yetu kuelewa kwamba tulitoa shilingi 500,000/= mpaka shilingi milioni 10 kwa sababu tulikuwa tunawaangalia watu ambao labda wanaweza wakaharibu kabisa kivuko.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali ije na jedwali, linaweza lisi- cover kila kitu, lakini angalau lioneshe msingi wa faini yake inayotolewa katika kifungu hiki na ile itasaidia kupunguza watu ambao wanafanya makosa madogo kutozwa faini kubwa au wanaofanya makosa makubwa kutoza faini ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja katika sheria ya Utumishi wa Umma. Sheria ya Utumishi wa Umma imempa nafasi Chief Secretary ya kusamehe conditions zote ambazo zinaweza kumsababishia mtu ashindwe kulipa mafao yake. Najaribu kutafsiri kwa Kiswahili ili niweze kueleweka, lakini kifungu kiko very clear.

Mheshimiwa Spika, sasa mwaka 2018 tumetunga sheria hapa ya Social Security ile ambayo ni almaarufu kama Sheria ya Kikokotoo, tukatunga na tukampa Waziri mwenye dhamana mamlaka. Tukatoka hapo, kuna Bodi ambayo inahusika na pension na mafao ya kustaafu.

Mheshimiwa Spika, sasa leo tukisema tunatoa mamlaka ya Bodi ambapo Bodi haiongozwi na mtu mmoja, tunatoa mamlaka ya Waziri, leo tunachukua nafasi ile tunampa Chief Secretary. Chief Secretary kwa Kiswahili anaitwaje kwani?

MBUNGE FULANI: Katibu Mkuu Kiongozi.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …tunampa Katibu Mkuu Kiongozi, ahsante. Tunampa Katibu Mkuu Kiongozi peke yake mamlaka ya kusamehe mazingira yoyote na imeandikwa kwenye act, mazingira yoyote ambayo yanaweza kufanya mtu asilipwe pension yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii sheria inayotungwa leo inakinzana na sheria ambayo tulitunga mwaka 2018. Kwa hiyo, naomba Serikali iweze ku-harmonize sheria hizi mbili kwa kuweka ama kurudisha mamlaka kwa Bodi ambayo iko chini ya Sheria ya Mifuko ya Jamii Na. 2 ya Mwaka 2018, irudishe mamlaka hayo na kwa minister. Sheria ile imeeleza bayana namna mamlaka haya yanavyogawanywa.

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa sheria ya ongezeko la thamani (VAT). Sheria hii Serikali kwa kweli imefanya vizuri kuondoa kodi kwenye miradi yote, fedha za miradi yote ambayo inahusisha Serikali. Hii wamesema vizuri kwamba inasaidia kuongeza kasi ya miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, nakuomba na niiombe Serikali ione haja ya kufanya hivyo hivyo kwa dhamira hiyo hiyo ya ku-speed up miradi ya maendeleo kwa private sectors. Najua hofu ya Serikali ni kwamba private sectors au watu wanaweza kutumia vibaya nafasi hii kujinufaisha wenyewe.

Mheshimiwa Spika, juu ya kifungu kile mwanzoni wanasema, “in consultation with the minister,” tena lazima ridhaa hiyo iwe published kwenye Government Gazette. Ile tu pekee inatosha kulinda watu wasitumie vibaya madaraka haya ya kutokutozwa kodi kwa vitu ambavyo wameingiza ndani ya nchi kwa ajili ya maendeleo au manufaa ya Umma.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kwenye Bunge hili lako Tukufu, wapo Wabunge ambao wanapewa vitu na wahisani na marafiki zao mbalimbali. Kuna watu wanaleta zile baiskeli za walemavu, kuna watu wanaleta pedi za kike, wanapewa na makampuni huko nje; basi hii iwe ni fursa kwao kuweza kuomba ridhaa ya Waziri wapate msamaha wa kikodi ili waweze kufikisha huduma kwa wananchi. Nchi hii ni yetu sote na tunaijenga wote kwa umoja wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kufafanua hayo, naiomba sana Serikali, ni mengi tumerekebisha kwenye Kamati, lakini bado tunayo nafasi ya kubadilisha zaidi, yawezekana mazingira yakawa ni magumu hasa kwenye suala la VAT, lakini dhamira ile ile ikitumika na njia ile ile ikitumika kuboresha misamaha katika miradi ya maendeleo kwenye jamii, Bunge lako ni Taasisi, Wabunge wako wana uwezo mkubwa wa kuweza kupata misaada kwa ajili ya kuwasaidia watu mbalimbali katika nchi hii, hii itumike kama fursa na VAT iondolewe katika miradi au katika misaada ambayo Wabunge wanapata, katika misaada ambayo Makanisa wanapata, katika misaada ambayo private sector wanapata kwa ajili ya kusaidia na kuwasaidia na kusaidia kusukuma gurudumu hili la maendeleo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Sheria ya Fedha ya Mwaka 2019
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mimi naomba nisiendeleze mjadala wa mawigi, wanawake wenzangu wamesema sana na nawaunga mkono japo mimi sisuki mawigi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichangie kidogo kwenye Finance Bill na nimkumbushe tu Naibu Waziri wa Fedha na Waziri wa Fedha kwamba mara nyingi mapendekezo mnayoyaleta ya kuongeza kodi au kuboresha mazingira ya kodi tangu nimeingia Bunge hili yamekuwa ni mapendekezo ambayo yana mtazamo wa muda mfupi. Pia, pamoja na kazi kubwa ninayoamini mnaifanya nyuma ya pazia, mnajipa muda mfupi kujitathmini uwezo wenu wa kutekeleza yale ambayo mmeyapendekeza. Hili limeonekana katika uondoaji wa VAT katika taulo za kike na katika mapendekezo mliyoyaleta mwaka jana na mwaka juzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nishauri tu kwamba Wizara ya Fedha inapoleta mapendekezo ya kodi kwanza ilete mapendekezo ambayo tuna uhakika ni endelevu lakini pili ijipe muda wa kutosha wa kujaribu mapendekezo yao na siyo mwaka mmoja kama wanavyofanya kwa sababu mwisho wa siku haileti tija na naamini rasilimali nyingi zinatumika, rasilimali fedha, muda na research zinafanyika kuweza kutuletea hapa mapendekezo haya, naamini hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niongezee kwamba tunayo changamoto kubwa na Waziri wa Fedha amekiri kwenye suala la vitambulisho vya wajasiriamali. Hili tulilisema tangu mwanzo wakati linaanzishwa na kwa bahati mbaya nafikiri sasa ni wakati muafaka Bunge litafute namna ya kufanya lobbying ya kuleta hoja nzito zenye maslahi makubwa kwa wananchi ndani ya jengo hili kwa sababu hoja inapoonekana imetoka upande wetu hata iwe nzuri kiasi gani watu wanaona ni bora tuipinge halafu tutakubaliana nao baadaye. Haya tutayaona hata kesho kwenye Muswada wa mabadiliko madogo ya sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Fedha amekiri kwamba mapungufu makubwa yako kwenye vitambulisho vya wajasiriamali na vitambulisho hivi havina jina, picha, saini ya mtoaji, haieleweki hizo pesa zinazokusanywa zinaenda wapi yaani hamna mfumo maalum na wala hatujui ni namna gani tutazifanyia audit pesa hizi.

Kwa hiyo, pamoja na Serikali kukiri kwamba kulikuwa na makosa fulani fulani wakati wa kutekeleza agizo hili la Mheshimiwa Rais, naomba zoezi la vitambulisho vya wajasiriamali lisitishwe kwa muda mpaka pale mtakapopata namna bora ya kukusanya mapato hayo maana tulishauri kwamba lisifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikufahamishe tu kwamba kitambulisho cha mjasiriamali kina bei kubwa kuliko kitambulisho cha Utaifa. Kitambulisho cha Utaifa kinatolewa bure, kitambulisho cha mjasiriamali unalipiwa Sh.20,000. Ukipewa kitambulisho cha Taifa unakaa nacho milele, ni cha kwako hakuna ku-renew lakini cha mjasirimali kinakaa mwaka mmoja. Kwa hiyo, niseme vitambulisho hivi vya ujasirimali iko haja kubwa…

T A A R I F A

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, kuna taarifa, Mheshimiwa Haonga.

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba hivi vitambulisho vina mapungufu mengi havina picha, jina kwa sababu mchakato wake haukuanzia Bungeni, ulianzia Ikulu na Wakuu wa Mikoa na Wilaya waliitwa kule. Kwa hiyo, vingeanzia Bungeni tungeshauri viwe na picha na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni taarifa tu ambayo nataka nimpe kwamba siku nyingine wakumbuke kwamba Bunge liko na linaweza likashauri namna bora ya kuweza kufanya mambo. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, endelea na mchango wako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru Mheshimiwa Haonga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemaliza kuhusu vitambulisho vya ujasiriamali na kitu ambacho napenda kushauri kwenye Bunge lako Tukufu ni kwamba visitishwe na ikibidi vikirudi vitolewe bure. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia kuhusu Sheria ya Ushuru wa Forodha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki…

T A A R I F A

MHE. MAULID S. A. MTULIA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome, kuna Taarifa nyingine, Mheshimiwa Maulid Mtulia.

MHE. MAULID S. A. MTULIA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kumheshimu sana mchangiaji lakini nilikuwa nataka kumpa taarifa ya vitambulisho vya wajasirimali vilikuja vikiwa ni mbadala wa kodi kubwa ambayo wajasiriamali walikuwa wakilipishwa, shilingi 500 kila siku. Kwa kupata kitambulisho kile wanalipa chini ya shilingi 50 kwa siku. Kusitisha kitambulisho kile maana yake ni kuwarejesha wajasiriamali kwenda kulipa shilingi 500 kwa siku kwa mwaka shilingi 180,000. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, namheshimu sana Mheshimiwa Mbunge wa Kinondoni lakini nimwambie kwamba Waziri wa Fedha amekiri vitambulisho vina mapungufu, hata wewe ni nani unataka kupotosha Bunge hili?

Mheshimiwa Naibu Spika, vitambulisho vya wajasirimali ushauri wangu ni kwamba vina mapungufu makubwa na Serikali imekiri na naishauri Serikali isitishe zoezi la vitambulisho hivi mpaka taharuki ya utekelezaji wa vitambulisho itakapotatuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee na Sheria ya Ushuru wa Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

T A A R I F A

MHE. SULEIMAN M. NCHAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, taarifa ya mwisho kwa Mheshimiwa Makamba, Mheshimiwa Nchambi.

MHE. SULEIMAN M. NCHAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mbunge anayeendelea kuchangia, anaonesha hisia za kutetea wajasiriamali lakini nataka nimpe taarifa hata madaktari wanapokuwa hospitalini, wanapokutana na challenge kwa mgonjwa huwa hawasitishi huduma ya mgonjwa bali wanamuweka pembeni halafu wanaanza kutafuta solution. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wakati tunatatua changamoto hizi, vitambulisho hivi vitaendelea kuwasaidia kwa sababu kabla ya vitambulisho hivi waliumia. Kwa hivyo, nilitaka tu nimpe taarifa mchangiaji, vitambulisho hivi akiri visisitishwe kwa sababu mwanzo kulikuwa na tatizo kubwa kuliko hili la hivi sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, malizia mchango wako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, huyo hakuwepo Bungeni tangu tumeanza Bunge la bajeti, kwa hiyo, alikuwa na hamu ya kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu sheria ya ushuru wa nondo, Serikali katika Muswada iliyoleta wanasema kwamba wameongeza bei ya ushuru kwa nondo zinazotoka nje ya nchi. Mimi nakubaliana na Serikali na measures wanazochukua. Kitu ambacho napenda kuishauri Serikali, watengeneze mazingira mazuri ya uzalishaji wa malighafi ndani ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipokuwa tunashauri kuhusu SGR na mradi wa Rufiji walisema kwamba kile chuma hakifai basi kitafaa angalau kwenye ndondo tujenge Mheshimiwa Waziri. Tunakuomba utusaidie ku-push mradi wa Mchuchuma na Liganga kwa sababu tutapata chuma cha kutosha ambacho kitatusaidia kushindana na vyuma vinavyotoka nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye mabomba ya plastiki. Haya nayo pia yamepandishwa kodi. Wewe ni shahidi, hapa Bungeni likiulizwa swali linalohusu maji safi na salama, Wabunge wote wanasimama na wanataka kujua hatma ya maji. Leo hatujawafikishia wananchi maji safi na salama na yanayotumika ni haya mabomba, hivi Serikali haioni umuhimu wa kuondoa kodi kabisa kwenye mabomba haya ili wananchi wapate maji safi na salama? Mimi sioni sababu. Juzi Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha wakati anahitimisha alisema kwamba kuna bidhaa ambayo ni ya msingi kwa wananchi kwa hiyo tusiwaadhibu kwa sababu ni lazima watanunua, bidhaa hii ipatikane ili watu wapate maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwa haraka kwenye incentive katika taulo za kike. Mimi nakubaliana na Serikali wamefanya utafiti wao wanasema kwamba walaji wa mwisho bei ya taulo haijapungua na wanasema kwamba wametengeneza mazingira ya kuleta viwanda. Tunayo miaka miwili ambayo wananchi na watoto wetu utu wao utadhalilika kwa sababu ya kushindwa kujistiri ili waweze kuhudhuria masomo. Serikali iwe sikivu iwasaidie tupate taulo hizi angalau bure kwa hiyo miaka miwili mpaka pale watakapoamua kwamba viwanda hivi vianze kufanya kazi na kuzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na 2) wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie mabadiliko haya madogo ya sheria mbalimbali yaani Miscellaneous Amendments (No. 2) Act, 2021).

Mheshimiwa Spika, nitaenda moja kwa moja kwenye vifungu ambavyo nadhani napenda kuishauri Serikali ivifanyie marekebisho. Pia nimeleta schedule of amendment kwa hivyo tutajadiliana na Serikali tukikubaliana watabadilisha.

Mheshimiwa Spika, Kifungu cha 4 cha Muswada ambacho kinabadilisha Kifungu cha 2 cha Sheria ya Mawakili kinasema, kutakuwa kuna Kamati ya Maadili ya Mawakili na kifungu hicho kinasema japo kwenye hotuba Attorney General hajasema, lakini sheria katika marekebisho inasema kwamba kutakuwa na Katibu wa Committee hiyo na Katibu huyo lazima awe mtumishi wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, sasa tusifunge namna hiyo, turuhusu Katibu nafasi itangazwe na apatikane katika hali ya uhuru. Akishapatikana anaweza kuwa enrolled na kuwa mtumishi wa Serikali. Hiyo itasaidia hata wale ambao ni Mawakili wazuri, ni Wanasheria wazuri kama vile Attorney General ameelekeza wanaweza kupata nafasi hiyo.

Mheshimiwa Spika, cha pili, Kifungu cha 10 cha Muswada ambacho kinarekebisha kifungu cha 17 cha Sheria ya Vizazi ya Vifo, kwa tafsiri isiyo rasmi, kinasema mwenza au mtoto au ndugu wa marehemu anaweza kwenda kuchukua cheti cha kifo cha marehemu huyo. Sasa kuna mazingira ambayo nadhani tumeyasahau, Tanzania ni nchi ambayo haifungamani na dini, lakini tufahamu kuna wenzetu Waislam ambao wana ndoa za mitaala, anaweza kuwa na wake wanne.

Mheshimiwa Spika, kama bwana Abdallah anaruhusiwa kuoa wake wanne, basi wale wanawake kama ana vyeti vya ndoa vine, basi anaweza kuwa na vyeti vikatengenezwa vyeti vinne vya kifo wakapewa wale wanawake na wasilazimishwe kwenda kukaa kwenye kikao kimoja wakati wengine wanaweza wakawa hawaelewani.

Mheshimiwa Spika, hiyo pia nimeweka kwenye marekebisho yangu, wapewe vyeti na watoto hivyo hivyo, kuna wakati inatokea…

SPIKA: Fafanua vizuri Mheshimiwa Salome.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, sawa.

SPIKA: Yaani hii foleni hakuna anayetangulia na anayefuata.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, sheria inasema kwa tafsiri isiyo rasmi kwamba, kama imetokea mwenza amekufa basi, mwenza wake anaweza kuchukua cheti chake cha kifo au mtoto au ndugu wa karibu wa marehemu, anaruhusiwa kuchukua cheti cha kifo. Mimi naifahamu scenario ambayo mke mkubwa alienda kuchukua cheti cha kifo akawanyima wake wenzake au scenario ambayo watoto ni wengi mtoto mmoja akachukua cheti wenzake wakakikosa na sasa hivi cheti cha kifo cha baba au cha mama siyo hiari, ukitaka kusafiri kwenda nje au kupata passport lazima ulete cheti cha kifo cha mzazi au cha kuzaliwa cha mzazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitaka kuomba mkopo kama ukitaka kusoma lazima ulete cheti cha kuzaliwa au cha kifo cha mzazi. Sasa kwa mazingira kama hayo unaweza ku- maintain registration number ya cheti cha kifo au cha kuzaliwa ikawa moja, lakini wale wake wa marehemu wote wapewe haki ya kupata vyeti hivyo ili kuepusha ule mgongano kwamba huyu amepata, huyu hajapata. Katika hili nilikuwa na hayo tu.

Mheshimiwa Spika, niende kwenye…

SPIKA: Nakushukuru tunao akina Mheshimiwa Bashiru, wako Maalhaji hapa, watatusaidia itakapofika wakati wa kujadili hapa kwamba katika mazingira haya sheria hii tunaitungaje? Endelea Mheshimiwa (Kicheko)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya hata definition ya spouse kwa maana ya spouse iliyoelezwa kwenye marekebisho ya sheria, hata kwenye sheria mama ya uzazi na vifo haijawa defined, hata kwenye tafsiri ya sheria pia haijawa defined. Kwa hiyo, kwa mazingira hayo complication ya jamii inayotuzunguka ndiyo inaleta hili ombwe ambalo naishauri Serikali ilizingatie.

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye marekebisho kwenye Muswada, Kifungu cha 17 kinachorekebisha kifungu cha 22 cha Sheria ya Usajili wa Majina ya Biashara(Tthe Business Name Registration Act), wanachoongelea habari ya online registration ya maombi ya biashara au kuuhisha biashara yako.

Mheshimiwa Spika, naelewa msingi wa Muswada huu na msingi wake mkuu ni kuiwezesha jamii ya Watanzania waweze kuingia kwenye uwekezaji ambao tunamwona Mama Samia anazunguka kuchochea wawekezaji ndani ya nchi, Watanzania tuweze kwenda kufanya biashara na kuingia kwenye mnyororo wa uwekezaji wa wawekezaji hawa wakubwa ambao wataingia. Sasa wote tunafahamu hapa, kila siku ukienda kwenye taasisi za Serikali iwe ni TRA, iwe ni Ardhi, iwe ni kwenye mambo sijui ya kuomba leseni, kila siku mtandao wa Serikali upo chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tuna karibu miezi miwili mtandao wa Serikali wa kupata hati tu za nyumba upo chini. Sasa hapa tunaongelea online registration za business registration tena jina tu la biashara wanasema tukafanye registration online, tunafunga mlango; yaani tunafungua mlango huu, tunafunga mlango huu; tunafungua wawekezaji, tunaweka masharti magumu ya registration ambayo ni online. Wakati huo huo haya mambo ya kuomba tenda za biashara, unataka ku-supply chakula kwenye makampuni makubwa, iwe ni kwenye bomba la mafuta, iwe ni kwenye Stigler’s Gorge haya mambo yana deadline.

Mheshimiwa Spika, tusipozingatia kwamba tuweke mazingira mazuri ya uwekezaji, mazingira mazuri ya kusajili makampuni Watanzania wataachwa nje. Kwa mfano mradi wa bomba la mafuta, wako Waganda mule, kuna kampuni za kimataifa, sisi tumekazana kujibana huko lazima kuwe na online registration inachelewesha muda, tunakosa fursa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hiyo tu kama Serikali imekubali kwenye Muswada huu huu, wamekubali wamesema badala ya mtu anayefungua kampuni kuleta kitambulisho cha NIDA wanasema tupeleke namba peke yake. Kwa mantiki hiyo hiyo waseme kama online registration imeshindikana, mtandao uko chini hauwezi ku-access computer, hujui kubonyeza, hujui kufanya nini, wapi unaweza kusajili kampuni yako ukimbizane na tender ambayo imetangazwa kwenye mtandao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye Kifungu 30 cha Muswada ambacho kimeongeza kifungu cha 3(5) hiki Kifungu ni hatari kweli kweli. Kifungu hiki kinasema:

“Mtu hataruhusiwa kufungua kampuni kama alishawahi kuhukumiwa …”

SPIKA: Mheshimiwa unasema Kifungu ni cha hatari?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ndio ni kifungu hatari sana.

SPIKA: Hebu subiri ni-sanitize kwanza maana yake eh!

Sasa unaweza kuendelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, unitunzie muda wangu tafadhali. Kifungu hiki kinasema; kama mtu aliwahi kuhukumiwa kwa makosa ya utakatishaji fedha, Human Trafficking mambo ya Money Laundering na kesi mbalimbali hizi huyo mtu hataruhusiwa kufungua kampuni, maana yake hataruhusiwa kufanya biashara. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mmeshanihukumu, nimeshatumikia kifungo, mnanitakaza kufanya biashara niende wapi? Niende wapi nikafanye biashara, lakini unafahamu na nilichangia Bunge lililopita humu ndani. Kuna haja kubwa ya kuleta mabadiliko ya sheria ya Pre-bargain ambayo tulipitisha ndani ya Bunge hili. Watu wengi wamelazimishwa kukiri makosa yao na kulipa fedha bila mchakato mzima wa kimahakama kufuatwa kuangilia beyond reasonable doubt kama wale watu kweli wana hatia. Wameamua wengine kukubali kwa sababu wamekaa jela muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, sasa kama mtu kakubali, maana yake huyo mtu ana hatia, halafu leo wanasema basi nilipoteza kingi nimelipa kwenye Pre-bargaining, nataka nikajaribu kuokotaokota kwa kufanya biashara, anaambiwa mtu huyo haruhusiwi kufungua biashara wala haruhusiwi kufanya biashara Tanzania kupitia kampuni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiki kifungu ni hatari na naomba Serikali ikifute kwa sababu hapa unamhukumu mtu kwa kosa moja mara mbili na unamfunga maisha yake yote asifanye biashara ndani ya nchi hii, ataenda wapi? Ipo haja kubwa sana ya kufuta kifungu hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Kifungu cha 39 cha Muswada, kifungu hiki kinasema, kimebadilisha Kifungu cha 455 cha Sheria ya Makampuni kwa kuongeza Kifungu kikubwa (A) kwa kusema kwamba mtu anatakiwa atunze kumbukumbu za nyaraka alizotumia kufungulia Kampuni kwa miaka 30. Sasa nafahamu kwamba Sheria ya Utunzaji wa Kumbukumbu inataka miaka 30, lakini hiyo sheria tuliitunga kabla hatujatunga sheria ya Serikali ya kuhamia kwenye mambo ya mtandao. Sasa hivi kila kitu kipo registered online, ukiweka ma-document yanakuwa uploaded online, unaniambia tena nikae na makaratasi miaka 30 tunataka ku-achieve nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeamua kufanya marekebisho ya sheria kama ni suala la kutunza kumbukumbu, nimeomba, nimeambatanisha vyeti, nimepeleka kwa Msajili wa Makampuni, vimeingia kwenye system, hiyo shughuli ya kutunza hizo kumbukumbu ibaki pamoja na Ofisi ya Msajili wa Makampuni na nisipewe tena burden kubaki na hayo makaratasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa haraka haraka niende kwenye mabadiliko ya sheria inaitwa The Land Disputes Courts Act, pale kwenye hii sheria wanasema kutakuwa na baraza ambalo linatengenezwa. Wametaja vizuri watu ambao wataingia kwenye baraza lile, lakini waliojaa kwenye baraza hilo ni watumishi wa Serikali, lakini kwenye hiyo Land Disputes Courts Act, wanaenda Mawakili wa kujitegemea.

Mheshimiwa Spika, Serikali haioni haja sasa kuingiza kipengele cha kuwajumuisha Mawakili wa kujitegemea kwa bahati nzuri wamesharasimishwa na Serikali inawatambua waingizwe pale kama sehemu ya wawakilishi.

Mheshimiwa Spika, tena nirudie Secretary (Katibu) wa Baraza lile, si lazima awe mtumishi wa Serikali, mtu yeyote mwenye uwezo wa kuomba, aombe, akipata kazi ya Secretary kwenye baraza lile, basi atarasimishwa na kuwa mtumishi wa Serikali, lakini msii-confine kuwa kwenye utumishi wa Serikali. Kwanza tumekubaliana humu ndani, watumishi wa Mahakama hawatoshi, sasa leo tunaanza kubana tena nafasi, mnataka muwachukue hao hao ndiyo wakawe ma- secretary. Tunataka efficiency, tunapotengeneza hizi forum tunataka efficiency na efficiency zinatokana na kupata watu ambao wana uwezo wa kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa heshima kubwa naomba tuzingatie hilo la kuweka Secretary na kuingiza Mawakili wa Kujitegemea kupitia Tanganyika Law Society wakawe sehemu ya baraza ambalo linatengenezwa kwa ajili ya Baraza la Ardhi la Wilaya kama linavyosemwa kwenye Muswada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema, kuna Kifungu ambacho kinahusiana na kuwaweka yaani Public Attorney, Government Attorney anaweza kuingia kwenye Mahakama za Mwanzo, lakini kinawaondoa kwenye ile orodha watu ambao wanaweza kwenye Mahakama ya Mwanzo kinawaondoa wale Court Assessors wanaitwaje kwa Kiswahili?

SPIKA: Wazee wa Baraza.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, sawa, Wazee wa Baraza, lakini kinawaondoa Wazee wa Baraza kwenye Mahakama hizi za Mwanzo. Sasa basi niwaombe Serikali, kama Mawakili watakuwepo ina maana part zote mbili zina uwezo wa kuwa na uwakilishi ambao ni competent. Naomba wakati ambao Mawakili hawapo, Court Assessors wawepo, kwa sababu kwenye Primary Courts zile Mahakama kesi ni za kawaida mno, mambo ya kijamii ya kawaida mno na watu wengi wanaopelekwa kwenye Mahakama hizi ni watu ambao hawana uwezo mkubwa wa kisheria. Logic, Mantiki ile ile iliyotumika kuweka Court Assessors iwarudishe hapo, nadhani Serikali ilipitiwa kidogo baada ya kuwaingiza hawa Ma-State Attorney na Mawakili. In absence of State Attorneys na Mawakili, basi hawa Ma-Court Assessors warudi katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Salome si ni Mjumbe wa Kamati.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, siyo mjumbe ila ukinirudisha huko nitafurahi sana. (Kicheko)
MUswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Usajili wa Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu wa mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi leo nichangie kuhusiana na sheria hii ya wahasibu na wakaguzi.

Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia siku ya leo, katika sheria hii nitarejea marekebisho ya kifungu cha 11 au ibara ya 11 ya muswada ambayo inahusiana na establishment of Accountants and Auditors Appeal Board.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Bodi hii ya Wahasibu na Auditors wametaja watu ambao wataingia kwenye Bodi na katika orodha hiyo wameweka watu katika mafungu matano; nikienda (a) wanasema; a chairman who shall be appointed by the President from among retired Judges or any person with qualification which may warrant such a person to be appointed as a Judge.

(b) Wakasema wataweka five members ambapo member wa kwanza atakuwa ni law officer ambaye ana represent Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali; member wa pili ni one senior member from the Ministry responsible for Finance; na member wa tatu ni one senior member from the Bank of Tanzania; wa nne ni senior member from Tanzania Revenue Authority; na wa tano hapa ndiyo kwenye ukakasi ni two members with knowledge and practical experience in accountant professional. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye kifungu hiki wameweka uwanja mkubwa sana wa Waziri kuchagua mtu yeyote ambaye ana elimu ya uhasibu anaweza kuingia kama member wa bodi, watu wawili hii ni hatari.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu nataka nishauri hapa, tunazo taasisi au vyama vya kitaifa vya wahasibu au watu wenye taaluma inayofanana na uhasibu ambao Waziri anaweza kwenda kuchagua members kutoka kwenye vyama hivyo, badala ya kupewa uhuru wa kuchagua mtu yeyote kwa sababu anaweza akaweka mtu yoyote hata rafiki yake, hata ndugu yake kwa sababu amepewa nafasi hiyo kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Kwa hiyo, ukisoma kwenye hotuba ya Kamati ukurasa wa pili viko vyama hapa ambavyo vimetusaidia kutuletea mapendekezo ya Kamati, kuna Chama cha Wahasibu Tanzania (The Tanzania Association of Accountants) au kuna Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) na vyama vingine vinavyofanana na hivi. Waziri apewe mandate kwenye sheria hii kwamba hao watu wawili atakaowachagua basi awatoe kwenye vyama vya kitaaluma vinavyofahamika kitaifa ili waweze kuingia kama members wa bodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ukiacha tu hivyo faida ya kuwachagua watu hawa wanapata uwakilishi, lakini wataweza kuwakilisha makundi makubwa ambayo yako nyuma yao, ni muhimu sana sheria hii ikazingatia jambo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye Ibara ya 12 ya muswada; Ibara hii ya 12 ya muswada imeleta mabadiliko kwa kufuta maneno yaliyokuwepo kwenye kifungu cha 25(1) cha sheria mama. Maneno yale yanasomeka ifuatavyo; wanasema, “The principal Act is amended in section 25(1) by deleting the words “and every order of the Appeals Board under this section shall be final, conclusive and binding upon all parties concerned, and shall not be subject to a review by any court.”

Mheshimiwa Naibu Spika, hiki kifungu kama ziko sheria zingine zilizo na kifungu hiki zinachozuia kwamba maamuzi ya Bodi ya Rufaa yatakuwa ndiyo maamuzi ya mwisho na hakuna chombo kingine chochote kitakachoruhusiwa kupitia maamuzi hayo. Hiki kifungu kinakinzana na Katiba, ukisoma Ibara ya 107(a) ya Katiba inasema; mamlaka yenye kauli ya mwisho ya utoaji haki katika katika Jamhuri ya Muungano itakuwa ni Mahakama.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumeleta mabadiliko ya muswada huu na ukiangalia kwenye mabadiliko ya muswada huu vifungu vinavyofanyiwa mabadiliko na kufutwa ni vingi mno, kwa maana hiyo kuna uwezekano kwamba ziko sheria nyingi kwa sababu hizi sheria imezeeka, ni ya mwaka 1972.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba kwa sababu tuko kwenye zoezi letu la uchangiaji ili tuweze kuingia kwenye Kamati ya Bunge Zima na kutunga sasa sheria. Hiki kifungu unachokisema hapa umeshakisoma kinasema mabadiliko kinayofanya kinataka haya yafutwe yasiwepo, maana yake hizi changamoto unazozisema zilikuwepo wakati yapo, sasa yanafutwa sasa hoja yako ni nini kwenye kufutwa haya maneno unataka yawepo au yaendelee kutokuwepo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, labda tu kwa vile naongea Kiswahili cha Kisukuma, unajua tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu hapa ni kwamba hii sheria ni ya mwaka 1972, ina miaka karibu 49 na ilikuwa na hiki kifungu humu ndani kinaishi. Hoja yangu kama sheria zipo nyingi za namna hii zenye kifungu cha namna hii, ipo haja ya Tume ya Mabadiliko ya Sheria kufanyia review ya sheria zote ili kuweza kuondoa vifungu ambavyo vinakinzana na katiba kama hiki ambacho kimeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi naunga mkono kukifuta hiki kifungu kitu ambacho kinanipa wasiwasi ni kwamba sheria hii inanipa ukakasi mkubwa, sheria hii imeishi miaka 49 ikiwa na kifungu kinachosema Bodi ndiyo itakuwa ina maamuzi ya mwisho, hivi fikiria sheria ngapi ambazo hazijafanyiwa review zina matatizo kama haya. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome nakubaliana na wewe kwa asilimia 100, lakini sasa kwa sababu tuko katika hatua ya kutunga sheria na sasa Serikali imeleta kifungu hiki wewe unaeleza kana kwamba viko mahali pengine ambayo ndiyo kazi yetu sisi kama Bunge ni kazi yetu wewe kama hapo unayo orodha ya hivyo vifungu wewe vitaje kwa sababu ukieleza kwa namna unavyoeleza sasa mimi nataka nikuongoze vizuri.

Muda adhimu wa Bunge unakuwa sasa huutumii vizuri, kwa sababu kifungu hiki ilicholeta marekebisho ni Serikali sasa ukianza kufikiri kwamba viko na vingine basi uvilete maana sasa hivi tunayotunga sheria ndiyo hii hapa, hata kama ina miaka 60, 40 lakini tunayotunga ni hii hapa na kifungu tayari kimeshafutwa. Sasa hapo tunalalamika au tunataka kifutwe yaani kiondoke kwa sababu ukizizungumzia sheria nyingine siyo tunazozizungumzia sasa hapa, tunazungumzia sheria hii, wewe kifungu hiki unatakaje? Ndiyo hoja.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee, katika sheria hiyo hiyo ya mabadiliko ya sheria hii hii kifungu cha 14 cha muswada kinafanya marekebisho ya kifungu cha 27 cha sheria mama ukienda pale (b) kwa hiyo inakuwa ni 14(b) kinasema; “deleting the closing phrase and substituting for it the following; (b) in the case of practicing firm, to a fine of not less than five million shilling or ten percent of the firm’s gross revenue, whichever is greater, provided that the amount charge shall not exceed thirty million shillings.”

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nishauri hapa kwenye kifungu hiki kama wana charge kiwango cha chini ni milioni tano, halafu wanasema au watampiga faini yule mwenye kosa watampiga faini asilimia 10 ya mapato ghafi, halafu wanasema asilimia 10 hiyo isizidi milioni 30; the shortcut is wangeandika tu kiwango kisichopungua five million na kisichozidi 30 million shillings, kwa sababu ukisema the greater value yaani it is over wording kwenye legal drafting unakuwa umeandika maneno mengi ambayo kimsingi ungeweza tu kuya-cover kwa kuweka tu ile 30 million na five million isipungue. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiachana na kifungu hicho ningependa pia kushauri katika muswada huu na mimi nakubaliana na mapendekezo ya Kamati cha kwanza nakubaliana na mapendekezo ya Kamati ambayo wameyatoa katika ukurasa wa 18 kuhusiana na kutenganisha majukumu ya NBAA yale majukumu ya regulation na majukumu ya kuwasajili hawa wahasibu na hii ndiyo practice, sasa hivi ilivyo kwa mujibu wa sheria na muswada huu mpya NBAA inawasajili wahasibu kwa maana ya kuwapa zile certificates, wakati huo huo inawasimamia wakikosea ina bodi ya kuwasimamia na mambo kama hayo. Sasa ni majukumu mengi ahalfu wakati huo huo yeye ndiyo anakuwa ndiyo referee na wakati huo huo ndiyo mchezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni nini kwenye hili; mimi nashauri NBAA kama ilivyo kwa upande wa taaluma ya sheria Law School ndiyo inayowa-train wanasheria na wanapata certificate ya practice wakitaka kuwa mawakili, lakini kwa upande mwingine TLS ndiyo ambayo inahusika ndiyo Chama cha Wanasheria; kusajili na kuwasimamia wanachama wao na mambo ya kinidhamu.

Kwa hiyo, ningeshauri hapa tutenganishe hizi function mbili ya regulation na registration kutoka NBAA wazitenganishe ili kupunguzia majukumu, lakini pia kuongeza ufanisi katika eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni hayo. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 7) wa Mwaka 2021
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia mabadiliko haya ya Sheria Na.7 ya mwaka 2022. Ikiwa ni mara ya kwanza kusimama mbele ya Bunge hili Tukufu napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kutujalia kufika mwaka huu salama.

Mheshimiwa Spika, niungane na Wabunge wenzangu kukupongeza kwa kushinda na kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kabla sijaanza kuchangia ningependa kumkumbusha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ni mpya, lakini sina wasiwasi na utendaji wake; kwenye hizi object clause, huku object and reasons, wameandika kwa Kiswahili na kwa kingereza, sasa Kiswahili kimeandikwa cha Kiingereza, wajitahidi kidogo wawe wanaandika Kiswahili fasaha, najua hilo halimshindi ili liende sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa manufaa ya watu wote kwanza kwa kujadili mabadiliko ya sheria inayohusiana na nolle prosequi. Kwanza nianze kwa kujaribu kuelezea neno hili kwa sababu, majirani zangu hapa wananiambia ni nolle prosequi au prose-cure au ni kitu gani?

Mheshimiwa Spika, kwa tafsiri isiyo rasmi nolle prosequi ni tamko analolitoa DPP mbele ya Mahakama baada ya, umekamatwa unapelekwa mahakamani leo, unarudishwa kesi imetajwa unarudi mahabusu au nyumbani. Unaenda tena kesho unarudi nyumbani. Keshokutwa DPP anasema kwa sababu nyingi ambazo ziko kisheria, anasema sioni sababu ya kuendelea na kesi hii uko huru. Sasa hiyo statement uko huru sioni sababu, ndio wanasema nolle prosequi.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa practice unaruhusiwa kwenda nyumbani, ukitoka nje, amesema vizuri kaka yangu pale, ukitoka tu pale nje unakutana na askari wanakukamata. Mara nyingi hii nolle prosequi, baadhi ya Waendesha Mashitaka huwa wanaitumia kwenye mazingira ambayo anaona kabisa amenikamata hakufanya upelelezi vizuri, hana namna yoyote ya kuni-convict na kosa ambalo ananishtakinalo, sasa ananitoa ili aweze kurekebisha vizuri makaratasi yake anirudishe tena mahakamani. Wakati anafanya hivyo ameshanipotezea muda wa kutosha kwenda mahakamani na kurudi au nimesota magerezani na mahabusu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu kwa kuiondoa hii nolle prosequi Taifa hili limepata ahueni kubwa sana. Vijana wengi sana hasa ambao wana mlengo ambao hauungani na Serikali huwa wanakamatwa na kuwekwa ndani kupitia kifungu hiki, umeshasota weee unaachiwa, hatuna kesi ya kuongea na wewe, uchaguzi umeshapita, matokeo umeshaibiwa, huna pa kwenda, unaambiwa nenda kapumzike nyumbani, sasa hii itakuwa mwarobaini.

Mheshimiwa Spika, kitu ambacho natamani Mwanasheria Mkuu wa Serikali atufafanulie, ameandika vizuri kwenye mabadiliko ya sheria kwamba, ataruhusiwa kwenda nyumbani na kama akikamatwa pale nje au dakika chache baadaye kwa kosa hilohilo, basi kosa hilo litaanzia pale lilipoishia.

Kwa hiyo, hakutakuwa na mambo ya kusota nenda na rudi. Akasema pia kama ni kosa tofauti lisiletwe mahakamani mpaka upelelezi utakapokamilika, sasa muda huo nitakuwa niko wapi? Niko mahabusu ya polisi, nitakuwa niko nyumbani nasubiria wamalize upelelezi au nitakuwa kusikojulikana? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali utusaidie, ili wasije wakawa wanaendelea kuwakamata vijana wetu huko. Tena safari hii watakuwa wanawakamata wanasema sikupeleki mahakamani upelelezi haujakamilika, sheria imesema utakaa mahabusu mpaka tumalize upelelezi, maana wanafanya hivyo. Najua kuna police bail, lakini wakati mwingine wanajificha kwenye kichaka hicho. Naomba tamko la mtoa hoja atakapokuwa anahitimisha alifafanue suala hili, itawasaidia sana Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ibara ya 24 ya Muswada inarekebisha Kifungu cha 47A(2) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai. Hiki ni kifungu hatari kwelikweli. Nasema hatari kwa sababu, kifungu hiki kinasema, Afisa Polisi Kificho hatahukumiwa au hatashtakiwa kwa makosa yoyote ya jinai ambayo atakuwa ameyatenda kwa kipindi ambacho alikuwa anafanya kazi kama Afisa Kificho.

Mheshimiwa Spika, kwenye mazingira haya ambayo Mheshimiwa Rais ametoka kusema Jeshi la Polisi…

SPIKA: Mheshimiwa Salome, Mheshimiwa AG nimekuona, naomba ukae kidogo. Mheshimiwa Salome kama umeisikiliza taarifa ya Kamati inaeleza kwamba, kifungu hicho kimefutwa kabisa. Kwa hiyo, kifungu hicho kimefutwa. Nilitaka nikueleze hiyo kwa sababu, marekebisho ya Serikali yako hapa kuashiria hilo; lakini Mwanasheria Mkuu wa Serikali ulikuwa umesimama ni hilo ulitaka kuzungumza?

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Ndio.

SPIKA: Basi sawa. Mheshimiwa Salome endelea na mchango wako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, mimi nakushukuru na ninakushukuru sana Mheshimiwa AG kufuta kifungu hiki, kwa sababu Mheshimiwa Rais amesema Jeshi la Polisi sasahivi linachangamoto ya uadilifu, linatuhumiwa kwa mauaji ya raia. Kwa mazingira kama hayo haiwezekani kile kifungu kingepita hapa Mheshimiwa Spika, kweli umeanza vizuri, umeupiga mwingi, umeanza vizuri, bora wamekifuta. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo nisipoteze muda, niende moja kwa moja kwenye mabadiliko ya sheria ya Baraza la Michezo. Sheria ile, bila kwenda kusoma kwa ajili ya muda, inasema chanzo cha mapato pekee, yaani mapato ghafi kwenye michezo ya kubahatisha (sports betting) kitapelekwa kwa ajili ya kusaidia Baraza la Michezo, kitapelekwa kwenye Baraza la Michezo.

Mheshimiwa Spika, haya ndio mambo tunasema hii nchi tuna tume maalum inaitwa Law Reform Commission, Tume ile kazi yake ni kufanya marejeo na marekebisho ya sheria zilizopitwa na wakati. Moja kati ya sheria ambayo imepitwa na wakati ni sheria ambayo sasa hivi inafanyiwa marekebisho. Sheria hii imeletwa leo, badala wailete yote kwa ajili ya kufanya marekebisho wameleta, wanaamini kakifungu haka kamoja tu ka mambo ya kuchukua pesa ile ya mapato ghafi ya michezo ya kubahatisha iingie kusaidia Baraza la Michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili Bunge ni Bunge la watu ambao wanafikiri sana kuliko hata wewe unavyoweza kuona. Kwa nini wasilete mabadiliko ya sheria? Mapato yanayotokana na michezo mbona yako mengi, ukiachana na hiyo sports betting? Siku hizi mtu anaingiza wimbo wake kwenye You Tube anapata millions of money. Watu wanapata views tu kwenye sijui Instagram, sijui ni nini, wanalipwa. Ukiacha hiyo juzi, nimemshangaa Mheshimiwa Mchengerwa anaenda eti kutoa mirabaha ya shilingi milioni nane! Unajua wale wasanii walikuwa wanamwangalia hawamwelewi na wala hawataki hiyo milioni nane kwa sababu, hawa watu wanapata pesa nyingi kuliko hata hiyo iliyoenda kutolewa kama mrahaba, yani wanapata pesa nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini msilete marekebisho ya sheria? Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali hii Law Reform Commission watu wako kwenye majengo, wanalipwa hela, wana magari ma-V8, wanafanya kazi gani kama hawaleti mabadiliko ya sheria? Mara ya mwisho wamefanya hii kazi mwaka 2002, miaka mingapi sijui iliyopita? Huyo mtoto aliyezaliwa kipindi hicho ameshaolewa saa hizi; kwa nini wasilete mabadiliko makubwa ya sheria tuweke vyanzo vingi vya mapato kutokana na sanaa inayokua katika nchi hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kwa kweli, pamoja na mabadiliko haya waliyoleta, lakini sijaridhika na review ya sheria hii inayohusiana na michezo, kuna pesa nyingi zinazopatikana. Siku hizi mtu wala hana haja ya kwenda kwenye kituo cha redio au TV kupeleka master yake ile ili mtu apige muziki, ukishaimba wimbo unaenda You Tube unaandika pale subscribe to my account, mtu aki-subscribe kule pesa zinaanza kuingia kwenye account huna wasiwasi. Hela inaingia, hulipi kodi, hulipi mrabaha, wala huhitaji mrabaha wala fadhila ya Serikali. Kwa hiyo, niombe Serikali ilichukulie jambo hili kwa uzito kwelikweli.

Mheshimiwa Spika, kwenye mabadiliko haya ya sheria, hii ya mwisho, nimeona, sijui kama Mwanasheria Mkuu alikuwa amedhamiria kufanya hivi au ni jicho lake limeteleza; wanafanya marekebisho, ngoja niangalie. Kifungu cha 29(4) wanafanya marekebisho kwa kuongeza kiwango cha fine kutoka milioni 10 mpaka milioni 300 kwenye Sheria ya Economic Organized Crime Control Act, Cap 200.

Mheshimiwa Spika, sasa hicho kifungu kinachofanyiwa marekebisho ukienda kukisoma…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja, malizia.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kifungu hicho kwa kifupi, bila kukisoma kwa ajili ya muda, hiki kifungu hakizungumzii kabisa masuala ya fine, wala hakizungumzii kabisa mambo ambayo Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameleta na ninacho hapa nitakuletea, kinaongelea utaratibu wa mtu kwenda kushtakiwa kwenda Mahakama Kuu, sheria hii hapa. Sasa hicho anachotaka kukibadilisha hapo mbona hakipo kwenye sheria mama?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, inawezekana wamepitiwa au wanarekebisha sheria nyingine ambayo mimi sina, lakini The Economic and Organized Crime Control Act, Cap 200, kifungu ambacho Mwanasheria Mkuu wa Serikali anataka kukibadilisha hakipo humu. Hicho kifungu anachokibadilisha kinahusiana na mambo ya procedure ya kushtaki kwenda Mahakama Kuu. Kwa hiyo, naomba wabadilishe hilo. Safari hii sileti schedule of amendment, nione kama watabadilisha. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa, 2022
MHE. SALOME WYCLIFFE MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie Muswada huu wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 1 ya Mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, nianze kuchangia kwa kunukuu kauli ya aliyekuwa Rais wa 16 wa Marekeni, Abraham Lincoln. Alipopewa nafasi ya kutafsiri nini maana ya demokrasia akasema demokrasia ni kutekengeneza Serikali ya watu inayotokana na watu wenyewe kwa ajili ya kuwahudumia watu hao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemnukuu Abraham Lincoln kwa sababu Serikali ya Chama cha Mapinduzi iko madarakani tunaamini kazi yake kubwa ya kwanza ni kuwahudumia watu; na katika Maisha yote mtu huhitaji huduma pale anapokuwa amepatwa na shida. Kwa hiyo, Sheria hii inayohusiana na maafa ni sheria ambayo itaonesha dhamira ya dhati ya namna gani mnaweza kuwahudumia watu wanapokuwa wamepatwa na shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utangulizi wangu huo unakwenda sawasawa na mabadiliko ambayo yameletwa kwenye sheria hii, Ibara ya 6, Ibara Ndogo ya 1(c) ambayo ilikuwa inaelekeza kwamba Serikali au Waziri ana uwezo wa kuchukua mali ya mtu yeyote pale ambapo ataona inafaa kwa ajili ya kwenda kuhudumia maafa.

Mheshimiwa Spika, wananchi ni mabosi zetu; na mimi naishukuru sana Kamati ya Katiba na Sheria kwa kuomba kifungu hiki kifutwe na nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri kuridhia kukifuta. Kuchukua mali ya mtu yeyote eti kwa sababu tena kwa namna Serikali au Waziri anavyoona inafaa huko ni kinyume na Katiba, ni uporaji wa mali za watu, ni jambo ambalo kiukweli lingetuweka pabaya sisi wawakilishi wa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye Sehemu ya Nne ya Marekebisho ya Muswada huu, ambayo kiukweli wameweka kipengele kinachohusiana na makusanyo ya pesa au fedha ambazo zitatumika kwa ajili ya kushughulikia watu ambao wamepatwa na maafa. Natamani sana, na ni kwa sababu ya muda, natamani sana tungekuwa na kifungu kidogo ambacho kinaruhusu fedha hizo zitakazokusanywa zitumike specific kwa kazi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi natoka Kahama. Miaka kama mitano saba iliyopita watu wangu wa eneo la Mwakata walipatwa na madhira makubwa sana ya kupata mvua ya mawe. Nyumba zao nyingi zilibomoka, watu walifariki na mifugo pia ilikufa. Fedha zilitolewa, wadau wakachangia, lakini mpaka leo kuna watu wanaishi ndani ya maturubai; zilipokwenda fedha zile hakuna anayefahamu. Vivyo hivyo, limewahi kutokea janga Nyangalata eneo la Kakola kule nyuma; watu walikaa chini ya ardhi kwa kufukiwa kwenye maeneo ya machimbo ya dhahabu kwa siku zaidi ya 40; na mimi nilikwenda kuwaona mwaka 2015. Fedha zilichangwa kwaajili ya watu wale akini re-allocation ya bajeti inafanyika pakubwa sana kwenye fedha za maafa. Wote tunakumbuka tulikuwa Bungeni tuliokuwepo kisa cha Kagera, wananchi walichangia tena kwa huruma kwa ajili ya kuwasaidia watu waliopata maafa, waliokufa na waliopoteza mali, mifugo na ndugu zao. Lakini fedha zile tuliambiwa zitatumia kwaajili ya kujenga shule, sijui barabara, sijui nini; na sasa watu wale mpaka leo wako kwenye simanzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ikimpendeza Mheshimiwa Waziri, fedha zitakazokusanywa kwa ajili ya maafa zifanye kazi ya kuwahudumia wananchi wanaopatwa na maafa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala hili hatujachelewa; liwekwe kwenye Kanuni, kwamba fedha ikikusanywa kwenye ngazi za kijiji, wilaya na mkoa zitumike kwa ajili ya wakati wa matatizo. Hapo tutakuwa tumekubaliana, kwamba Serikali ipo imewekwa na watu kwa ajili ya maslahi ya watu wale.

Mheshimiwa Spika, wote tunafahamu kwamba tunapofikwa na maafa ni jambo la dharura; na tuseme tu katika hali ya kawaida Serikali inawahudumia wananchi karibu kila siku. Lakini kwa vile tumeona suala la maafa ni la dharura tumetengeneza timu maalum. Lakini hivi kweli kamati ya kitaifa, sijui kamati ya wilaya, mara ya wataalam; jukwaa la wadau, watu zaidi ya 113 wanatakiwa wakutane ili waweze kupanga jambo la dharura. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, umuhimu wake ni nini? Kama Serikali ipo, tutengeneze Kamati ya Dharura ambayo inaweza ikakutana kwa dharura na kufanya maamuzi ya dharura kwa ajili ya maslahi ya dharura. Hii ya kusema sijui na nani ameingia, hii siyo fursa. Hatuendi kutengeneza taasisi ili watu waweze kunufaika; huyu amekuwa Mwenyekiti, Mkurugenzi wa Maafa, huyu sijui ni Makamu Mwenyekiti, hapana. Tutengeneze task force ambayo inaweza ikakutana kwa dharura, ikafanya maamuzi kwa dharura na watu waweze kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Muswada huu Ibara ya 8 mpaka ya 11 naona ni ibara ambazo zinataka kutengeneza ukiritimba (bureaucracy) ambao hauna maana yoyote wala umuhimu wowote na mwisho wa siku unaweza ukashangaa Kamati ya Wataalam inakwama kwa sababu huku Kamati ya Mawaziri haijakaa. Mara jukwaa la wadau linakwama kwa sababu kuna Chama fulani sijui hakijaingia, hakijasikiliza au hakijafanya nini. Naomba suala hili lisichukuliwe kama fursa, lichukuliwe kama lilivyo kwenye sheria. Ni suala la maafa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Ibara ya 39, eti inasema: “Waziri atatengeneza Kanuni kuhusu suala lolote ambalo ni lazima kwa madhumuni ya utekelezaji wa sheria hii. Uzuri, Wanasheria wako wengi humu ndani. Hatuwezi kutengeneza sheria ya jumla namna hii. Yaani Waziri atengeneze Kanuni kuhusu suala lolote ambalo anaona yeye linafaa! Ni lipi hilo ambalo sisi Wabunge 400 na kitu humu ndani hatuwezi kuliona? Kama kunatokea ulazima wa kuleta suala hilo, liletwe Bungeni. Wanaotunga Sheria ni Wabunge, sio Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hatuwezi kutengeneza kifungu cha jumla na ndiyo maana kule kwenye Kanuni imewekwa pale Ibara ndogo inasema: “Waziri atatengeneza Kanuni ili kuweza kutekeleza kifungu cha juu. Sasa hiki kifungu kimesimama chenyewe, kinampa mwanya Waziri. Sisemi Mawaziri wetu ni wabaya, lakini anaweza kukaa hapo kwenye kiti mtu ambaye hana nia nzuri akatengeneza sheria yoyote ambayo itasaidia lolote kuhusiana na maafa. Hiyo sheria ni ipi ambayo ipo general kiasi hicho? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ikikupendeza, naamini busara yako, ya Kiti, kifungu hiki kimekuwa too generous na kinakwenda kinyume hata na Kanuni na taratibu za utungaji wa sheria. Kwa maana hiyo, kifungu hiki kinaweza kikafutwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ibara ya 38 ya Muswada inasema hivi: “Mtu yeyote ambaye kwa mujibu wa sheria hii au kanuni ameruhusiwa kushiriki katika utekelezaji wa masharti ya sheria hii, hatashitakiwa binafsi kwa jambo lolote alilolitenda au kuacha kutenda kwa nia njema wakati akitekeleza shughuli hiyo ya usimamizi wa maafa.” Hivi tunapimaje nia njema ya mtu? Ni mara ngapi tumeona viongozi wa Serikali tena Waandamizi wanafanya maamuzi ya kizembe yanayopelekea ulemavu kwa Watanzania, yanayopelekea upotevu wa mali kwa Watanzania, yanayopelekea dhuluma na ukatili kwa Watanzania? Ni mara ngapi? Leo tunakwenda kutengeneza kifungu kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu umekuwa ni utaratibu. Nadhani viongozi wa Serikali wameshagundua kwamba kuna wakati wanafanya mambo kwa uzembe, na kwa sababu principle ya kukiri makosa na kujiuzulu hawataki kwenda nayo, wanatengeneza vifungu vya sheria ambavyo vinawalinda kwa maamuzi ambayo ni ya uzembe wanayoweza kufanya. Hili suala halikubaliki. Kama kosa limefanyika, kama maafa yametokea, itatengenezwa timu maalum ya kufanya evaluation ya namna Serikali, Waziri na Mkuu wa Mkoa alivyotekeleza majukumu yake katika kushughulikia suala hilo. Ikionekana kuna uzembe wowote ambao umefanyika, kila mtu atabeba mzigo wake. Kila mtu abebe mzigo wake. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani mtu anafukiwa kwenye shimo siku 40 lakini Serikali ipo. Halafu leo unasema eti hatashitakiwa kwa sababu alikuwa anashughulikia maafa. Ashitakiwe, awajibishwe na ikibidi yule aliyehusika na hayo maafa alipwe fidia. Kwa hiyo, sikubaliani kabisa na hii trend ya Serikali ya kuleta vifungu vya kuweka kinga dhidi ya uwajibikaji au uzembe unaoweza kujitokeza kutokana na wao kushindwa kutekeleza majukumu yao. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, mimi niseme, sheria inaweza ikawepo na tukatunga nzuri, lakini lazima tukubaliane, Sheria Sura 242 inayofutwa ilielekeza kwamba lazima kuwe na fungu kwa ajili ya maafa. Ilielekeza clear, lakini fedha zilikuwa hazipelekwi. Kwa hiyo, ni kuhusu utashi wa kisiasa wa kuona kwamba wananchi ni mabosi wetu, ni lazima tuwasaidie, nasi kama viongozi lazima tuwe na moyo wa kibinadamu. Tunaweza tukaweka sheria nzuri, bajeti itengwe, ikatengwa na isipelekwe. Tukaweka sheria nzuri, fedha ziwe-ringfenced, wakatokea viongozi ambao wanajiona kwamba wao wako juu ya sheria, wakatumia vibaya fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, laiti kama, na ninajua wengi humu tumewahi kulalamika hata tunaleta hoja za dharura; ukiona watu wanavyoteseka wanapopatwa na majanga, sisi Wabunge tunaweza kuwa tuna-privilege, lakini fedha zinazotengwa ziende kwenye mfuko. Tusizichungulie zile fedha kutaka kuzidokoa dokoa hatuwezi kujua ni jambo gani linaweza likatupata muda gani ili tuweze kulishughulikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru. Naomba kuwasilisha. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Salome Kifungu kinachotoa mamlaka ya jumla kwa Mheshimiwa Waziri kutunga Kanuni, umeshaleta marekebisho hapa mbele au Hapana!

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, Hapana, sijaleta.

SPIKA: Sawa. Ahsante sana.
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (no. 2) Act, 2022
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nichangie Muswada huu Na.2 wa Mwaka 2022 ambao umeleta mabadiliko ya Sheria tatu; Sheria ya Usafirishaji wa Binadamu, Sheria ya najaribu kutafuta kwa Kiswahili jana umetusisitiza sana, imebidi niandike pembeni.

MBUNGE FULANI: Ongea tu lugha ya malkia.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, sawa. Sheria ya Anti- trafficking in Persons Act; Sheria ya Drugs Control and Enforcement; na Sheria ya mwisho ni Sheria ya The Public Leadership Code of Ethics. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ya leo imeletwa ya Kiingereza kwa hiyo utaturuhusu tu tusome yaliyoandikwa humu ndani kwa Kiingereza. Nianze na Sheria hii inayohusiana na dawa za kulevya. Wote tunakubaliana humu ndani kwamba changamoto ya matumizi ya dawa za kulevya ni kubwa sana na sijamsikia hata mmoja Mbunge mwenzangu aliyekataa kwamba wanaohusika na uuzaji wa dawa za kulevya ni ma-tycoon, ni watu matajiri; ni watu ambao wameshikana na mfumo. Tukubaliane tu Waheshimiwa Wabunge, kuna madhara makubwa wamewahi kuyapata baadhi ya Wabunge wenzetu ambao walikuwa wanapinga au wanajaribu kuwatetea wananchi dhidi ya matumizi ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Spika, amesema vizuri sana mjomba wangu pale Mheshimiwa Mpina, lakini nafikiri hakusoma vizuri mabadiliko ya sheria; kuhusiana na hizi Selo au Mahabusu; Sheria inasema hivi: Ibara ya 13(3) ya Muswada, inasema: “The Officer of the Authority shall, in exercising the power under the subsection (1) and (2) and where the circumstance is so required, consult and cooperate with other relevant authority.”

Mheshimiwa Spika, maana yake nini? Mamlaka wakati wanatekeleza majukumu yao ni lazima washirikiane na mamlaka zingine na naamini mamlaka hizo mojawapo ni Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ikaenda mbele kifungu kidogo cha (4) ikasema: “For the purpose of exercising the powers referred to under subsection (2), the Authority may establish cells or facilities for keeping a person arrested under the Act.”

Mheshimiwa Spika, hapo ndiyo pameshikiwa hapo kwamba wataanzisha mahabusu, lakini Kifungu Kidogo cha 5 ndiyo kinafafanua zaidi kinasema: “The safety of the person detained under subsection (4) and other matters relating to sending such person before the court shall be as provided for under the written laws.”

Mheshimiwa Spika, tunaongelea watu kukamatwa ambao mchakato wake umekuwa ni mgumu kweli kweli kuwakamata hao wahalifu. Hata hivyo, wakikamatwa wanapelekwa kwenye mahabusu zetu na wengi wanatorokea hapo. Sisi tunafikiria namna bora ya kuzuia wasitoroke kwa maana taarifa zinavujishwa, vielelezo vinapotea, watu hawa wawekwe kwenye mahabusu maalum. Kama hiyo haitoshi watu wengi wanaokamatwa au wanaosafirisha haya madawa teknolojia sasa hivi inaonesha usafirishaji ni hatarishi zaidi kwa maisha yao kuliko hata dawa zenyewe.

Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo hawa watu ni lazima wawekwe kwenye uangalizi maalum ndiyo maana ya facility; wanawekwa kwenye uangalizi maalum ili kusudi kwanza tumesikia alifariki Msanii Mangwea, yale madawa yalikutwa tumboni na yakatolewa yako tumboni. Sasa imagine kwenye mahabusu za Polisi za kawaida na kama mtu huyo angeweza kupelekwa kwenye eneo maalum, pengine tungeweza kuokoa uhai wake. (Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Spika, lazima tukubaliane vita ya madawa ya kulevya ni vita ngumu na mwisho wa siku Polisi ndiyo wanaoongoza kwa kuvujisha taarifa za wauzaji wa madawa ya kulevya. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Spika, mwisho wa siku Vituo vyetu vya Polisi havina mazingira mazuri ya kuweza kumsaidia mtu ambaye anasafirisha dawa za kulevya ambaye wakati mwingine anafanya kwa shinikizo la ujinga, umaskini au la watu wanaomzunguka. Kwenye hilo, naunga mkono kwa asilimia mia moja. (Makofi)

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Salome ngoja twende vizuri, nani amesimama kuhusu taarifa? Subiri kidogo Mheshimiwa Kigwangalla.

Mheshimiwa Salome nilikuwa nasikiliza hapa kwa makini kwanza umemtaja huyu aliyekuwa msanii ambaye ametangulia mbele za haki. Hii taarifa unayoisema mimi binafsi sikuwahi kuiona mahali, ni taarifa rasmi, iko mahali kwamba alifariki kwa sababu ya madawa yalikuwa tumboni, ndiyo sababu ya kifo chake, maana sitaki tufike mahali ambapo tutaanza kuulizana haya mambo, maana sheria zetu zinatulinda sisi Wabunge na zinawalinda na watu wengine. Hii ni taarifa mahsusi unaitoa wewe ama ni taarifa mahsusi ambayo Serikali imeitoa kwenye Kamati yenu wakati ikionesha umuhimu wa jambo hili? Nataka tu kujiridhisha na hilo maana sitataka kuletewa kesi hapa kwamba, marehemu amesemwa vibaya. Hizo taarifa mimi sizifahamu ndiyo nazisikia kwako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, marehemu hasemwi vibaya, it was all over the news, Vyombo vya Habari viliandika ambapo ni formal na visivyokuwa formal, kwa hiyo…

SPIKA: Sasa ngoja ngoja kwa hapa Bungeni ili lisemwe kwa namna hiyo lazima mimi nijue kama hiyo ndiyo sababu ya kifo ambayo imetajwa; maana kila mtu jamani sababu ya kifo si huwa inatajwa. Kama hiyo siyo sababu hayo maelezo kuhusu Mangwea, naomba uyaondoe ili tubaki na hiyo taarifa ambayo ndugu zake watakuwa nayo.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, sawa.

Jambo la pili, kabla sijamruhusu yule wa kukupa taarifa ni hii ya polisi, kwamba ndio wanavujisha taarifa za wale wenye tuhuma za dawa za kulevya wanavyokuwa kwenye remand zao. Hilo nalo nataka kujua Waziri wa Nchi uko hapa, ni polisi ndio anavujisha hizo taarifa? Yaani Bunge linataarifiwa kwamba polisi ndio wanaotoa hizo taarifa ama! Nataka tu kujiridhisha ili baadaye chombo chetu cha polisi tusije tukakiweka mazingira kwamba watu wanapelekwa huko halafu chenyewe ndicho kinasababisha utekelezaji wa sheria uwe mgumu.

Mheshimiwa Salome ili tuliweke vizuri ngoja Mheshimiwa Waziri wa Nchi amesimama.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, URATIBU NA BUNGE: Mheshimiwa Spika, kama nimemuelewa vizuri Mheshimiwa Salome alichokizungumza amezungumzia juu ya complexity ya namna ya upatikanaji wa ushahidi unapotuhumiwa mtu ambaye anasafirisha au anatuhumiwa kwa namna nyingine yoyote au anatuhumiwa kwamba amebeba dawa za kulevya ndani ya mwili wake; kwamba mazingira yale ni very special. ndicho nilichomuelewa akiwa analizungumzia. Kwamba pengine katika mazingira yale si rahisi kwa mazingira ya vituo vyetu vya polisi kuweza kuwa na mazingira ya namna hiyo. Kwa sababu, hizo special facility zinaweza zikawa hazipo na yule mtu anaweza akawa hajapata fursa nzuri na kwa hivyo tusipate ushahidi unaokusudiwa. Kwamba polisi wanavujisha hili ni jambo lingine sasa ambalo nadhani…

SPIKA: Basi Mheshimiwa Waziri utakuwa haukumsikia vizuri maana unayotoa wewe ni yale uliyotoa taarifa kuhusu Mheshimiwa Mpina. Yeye Mheshimiwa Salome anaunga mkono kabisa kutengenezwa hayo mazingira mahususi kwa ajili ya hawa ambao ni watuhumiwa wa dawa za kulevya, anaunga mkono hoja hiyo. Hoja yangu mimi ni pale ambapo kwenye lugha ya mazungumzo anasema; kwa kuwa hawa watuhumiwa wanapelekwa polisi kwenye remand zile za kawaida, polisi ni sehemu ya watu ambao wanatuhumiwa kuvujisha taarifa zinazowahusu wale watuhumiwa. Kwa hiyo, tusikilize vizuri ili Bunge letu lisije likakaa na taarifa ambazo kidogo zitatufunga sisi wenyewe hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo kuna watumishi ambao si waadilifu, baadhi, kwa sababu haiwezi ikawa wote mwisho wa siku kuna wengine wanafanya vizuri wengine wanafanya vibaya. Lakini kwenye mazingira yanayohusiana na dawa za kulevya wapo askari polisi ambao wanahusika moja kwa moja kwa ajili ya kuvujisha taarifa, ili kuweza kumlinda aidha yule anayesafirisha madawa ya kulevya au yule aliyemtumia nafasi yake kuuza madawa ya kulevya [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sio wote lakini wapo ambao wanahusika kufanya hivyo wanaweza wakawa sio wote. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Salome. Kilichozungumzwa ni kwamba, si kutokuliamini Jeshi la Polisi. Hayo anayosema yeye ni hayo lakini kilichozungumzwa na kujadiliwa ni kwamba wale wanaoingia kwenye mahabusu za polisi ambao ni watuhumiwa ndio wanaovujisha hizo habari na kukosa kupatikana ushahidi wa sehemu nyingine ambayo inatakiwa zikakamatwe hizo dawa. Hivyo ndivyo tulivyokubaliana.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nilipenda kumpa taarifa Mheshimiwa Salome Wycliffe Makamba, kwamba hata kama zitakuwepo mahabusu maalum ambazo zitakuwa zinasimamiwa na hii Mamlaka ya Kudbiti Dawa za Kulevya, huo wasiwasi alionao, kwamba kuna polisi ambao wana changamoto ya kuvujisha taarifa za watu wanaofanya biashara ya dawa za kulevya; kwa kuwa hata huku kwenye chombo hiki cha mamlaka wanaofanya kazi ni binadamu ni Watanzania wenzetu na hawako perfect vile vile yanaweza yakajitokeza na huku pia.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, kwa kuzingatia muktadha kwamba wanaofanya kazi kwenye hivi vyombo ni binadamu, ni Watanzania wenzetu asitumie lugha ya kujenga hoja ambayo inalituhumu moja kwa moja Jeshi la Polisi na Askari wetu, chombo ambacho tunakiamini na tunakitegemea katika kusimamia usalama wa raia kujenga hoja ya uhalali wa kwamba basi tuwe na chombo hiki pengine hiki kitakuwa waterproof. Kwamba kitakuwa kina watu ambao ni wazuri zaidi kuliko wale polisi kwa sababu wote ni binadamu. (Makofi)

SPIKA: Sawa; sasa Mheshimiwa Salome kabla sijakupa fursa ya kuipokea ama kuikataa taarifa hiyo kwanza, nimeendelea kutoa maelezo pamoja na wewe kutoa ufafanuzi wa kusema si wote ni baadhi. Ukishasema baadhi kwa sababu tunazungumzia chombo ambacho kinasimamia usalama wa raia, hata hao baadhi tutataka kujua kama ushahidi upo ama haupo. Kama ushahidi haupo hili la baadhi liondoe wewe endelea kujenga hoja yako. Kwamba, kwa nini kuna umuhimu wa kuwa na hizi mahabusu maalum kwa ajili ya watu hawa ndio hoja yako ya msingi. Hawa wanaovujisha sijui akina nani, baadhi; kama hatuna ushahidi hasa wa kwamba kuna polisi ambao wamewahi na wenyewe sasa baada ya kuvujisha wakatuhumiwa, hilo tuliondoe kwenye taarifa zetu rasmi halafu wewe jenga hoja yako ambayo ulikuwa umeanza nayo tangu mwanzo. (Makofi)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniongoza, na nimuombe Mheshimiwa Kigwangalla asinilishe maneno mdomoni. Kama alikuwa anataka kuchangia achangie ya kwake lakini asinilishe mimi maneno ya mambo ya uadilifu na kutegemea Jeshi la Polisi. Kwa sababu, hata mimi najua umuhimu wake na siwezi kusema hivyo ulivyosema wewe kwa hiyo sikubali mchango wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizane na hoja ya dawa za kulevya hakuna kipya ambacho tunakifanya.

SPIKA: Ngoja ngoja umefanya vyema taarifa yake umeikataa sasa rekebisha yale maneno yako yafute yale kama ulivyofuta ya Mangwea halafu muda wako mimi naulinda usiwe na wasiwasi.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nimeyafuta naomba niendelee samahani sana.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, hakuna jambo jipya ambalo tunalifanya kuhusiana na kuanzisha cell/remand au special facility kwa watu ambao wanaathirika na madawa ya kulevya. Katika East Africa Rwanda na Kenya wanafanya. Duniani Italy, Marekani, India na Brazil; na nchi kibao wanafanya. Kwa nini wanafanya hivyo, ni kwa sababu ya unyeti wa jambo hili na wahusika wanaohusika na mambo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoka hapo niende kwenye Sheria ya Usafirishaji wa Binadamu. Nimeona tunajaribu kuongeza kiwango cha adhabu kwa maana ya kifungo na faini kwa watu wanaohusika na usafirishaji wa binadamu. Mimi sijui ni kwa nini Serikali hawajaliona hili kwa uzito kama walivyoliona la dawa za kulevya, sijui ni kwa nini. Biashara ya usafirishaji wa binadamu ilishapigwa marufuku miaka mingi iliyopita, hatuna sababu yoyote ya kuendelea kubembeleza watu wanaosafirisha binadamu. Kusafirisha binadamu ni unyama.

Mheshimiwa Spika, juzi nimeona kwenye taarifa ya habari, kuna mtu amesafiri sijui kutoka Mbeya kakaa kwenye lile buti la basi. Hivi fikiria wewe ukae kwenye buti la basi kuanzia asubuhi mpaka jioni eti unasafirishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ridhaa yako mimi nafikiri hivi viwango vya fine vilivyowekwa; kwanza hakuna sababu ya kutoza eti faini ya Shilingi milioni 50. kwa sababu kama mimi nataka kusafirisha binadamu nawapeleka nje kwenda kufanya kazi ambayo mtu mmoja analipwa kuanzia dollar 5,000 mpaka dollar 15,000 hivi kweli faini ya Shilingi milioni 50 ni kitu gani? Faida wanayoipata hawa watu wanaofanya human trafficking ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, mwisho wa siku ninachoshauri, ningependekeza kuwe kuna kifungo cha maisha kwa watu watakaokutwa wanafanya shughuli ya kusafirisha binadamu. Na ukiacha hivyo, kusiwe na faini, kwa sababu faini tunatengeneza majadiliano. kusiwe na faini yoyote kuhusiana na kosa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Sheria ya mwisho ya Maadili ya Utumishi wa Umma. Sheria hii ya Kanuni ya Maadili kwanza, sijui labda inawezekana wamepitiwa; wanarekebisha kifungu ambacho hakipo. Wanasema sehemu ya nne ya Muswada sheria inarekebisha kifungu cha 9 (1)(c) kwenye sheria inayorekebishwa hicho kifungu hakipo nataka kuamini kwamba walipitiwa kwa sababu kuna (a) na (b). Sasa, hicho kifungu cha (c) ambacho kinabadilishwa wanaongeza kwa kusema eti mtu anapoacha kazi anatakiwa kujaza ile fomu ya maadili angalau miezi mitatu kabla hajaacha kazi. Sasa kipindi cha mwendazake tulikuwa tunaona mtu ukienda kwenye mkutano wa hadhara unatumbuliwa sasa hiyo miezi mitatu nyuma utaipata wapi ya kujaza fomu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaona kuna watu wanaachishwa sijui watumishi hewa angepata wapi muda wa kujaza fomu nadhani hapo mmesahau kidogo, hiyo sifa ya kwamba ujaze miezi mitatu kabla ama iondolewe au iboreshwe kwa mazingira kama hayo ya mtu ambaye hatopata hiyo nafasi ya kupata miezi mitatu kabla ya kujaza fomu ya maadili.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, Sehemu ya nne, Ibara ya 20 ya Muswada inarekebisha kifungu cha 11(2) ambayo inaongeza wigo wa mali zinazotakiwa kuorodheshwa na mtu ambaye anatakiwa kujaza fomu ya maadili. Wote tunajua huwa tunajaza mashamba gari nini, sasa zamu hii kwa kweli Mheshimiwa Attorney General umeleta kichekesho. Umeleta kichekesho kwa sababu meongeza katika mali zinazotakiwa kuongezwa eti tuzijaze ni hizi zinaitwa household goods. Sasa nimeenda kwenye tafsiri ya sheria kuangalia maana ya…

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Najma Giga.

T A A R I F A

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Salome, inawezekana hajaisikiliza vizuri taarifa yetu ya Kamati. Ni kwamba Serikali wameshakubali na wamekiondoa hicho kifungu kwa hiyo wameona hakina maana. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Salome Makamb, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Najma taarifa yako naipokea lakini kwa manufaa ya wengi ambao hatukuwepo kwenye Kamati walikuwa wameweka kitu kinaitwa household goods. Household goods zinahusisha nilienda kwenye google tuliambiwa tu-google inahusisha wanyama wale nyau, mbwa wa pale nyumbani kwako, mabakuli, vitanda. Sasa tuna kitu kinaitwa admin means rule… (Makofi/Kicheko)

T A A R I F A

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuwa hiki kifungu kimefutwa nafikiri Mheshimiwa Salome anajaribu kuweka msisitizo ili kisije kikarejea tena humu Bungeni. Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. (Makofi/Kicheko)

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, lengo langu ni kulinda hadhi ya mwenendo wa majadiliano ya Bunge kitu kikishaondolewa hakipaswi kuingia kwenye kumbukumbu.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ni kweli Mheshimiwa Attorney General mimi nakumbusha tu ili tuongeze umakini kwa kweli taaluma ya sheria, tunatumia muda mwingi sana kusoma na kwa kweli sikutegemea kama tutakutana na mambo kama ya nyau. Kwa hiyo, niombe tu tuongeze umakini kwenye eneo hilo kwa sababu nakuamini sina wasiwasi na wewe na ndiyo maana ulikubali that is household goods haiwezekani. Mimi nakubaliana na mabadiliko ya sheria lakini nakushukuru sana. (Makofi/Kicheko)
The Water Resources Management (Amendment) Act, 2022
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba nitofautiane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuhusiana na mapendekezo yaliyoletwa mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ni kijana na nilikuwa nategemea kwa ujana wake angeisaidia Serikali kuwafikia wananchi kwa kuwapelekea maji ya kutosha; pia angeisaidia Serikali kufanya maji kuwa sehemu ya mchango mkubwa wa kuingizia Serikali kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Ibara ya 10 anasema, mtu akitumia maji kupita kiasi alichoruhusiwa kutumia anatenda kosa na unampa adhabu takribani mpaka Shilingi milioni 10 au kifungo cha miezi sita. Mheshimiwa Waziri usiturudishe huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo ya kutupimia kiasi cha maji cha kutumia yalikuwa ni mwaka 1980 huko ndiyo mtu alikuwa anaenda kuchukua sukari kwenye duka la Ushirika; anapimiwa sukari kilo mbili kwa sababu ana watoto wawili. Acha watu watumie maji. Unachotakiwa kufanya ni kupima units za mtu anazozitumia na kum-charge kwa unit kama wanavyofanya watu wa umeme. Usimwambie mtu eti katumia maji mengi, hivyo anatenda kosa, unataka umfunge jela miezi sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wanaosema eti kuna vita, sidhani kama kutakuwa na vita kubwa kama kumfunga jela mtu ambaye anatumia maji kwa ajili ya familia, anatumia maji kwa ajili ya kukuza uchumi na ustawi wa familia yake, eti unamfunga jela kwa sababu kazidisha kile kiwango ulichomruhusu kutumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anasema hapa eti ni kosa mtu kubadili matumizi ya maji kutoka kwenye kile kibali alichopewa. Hivi mimi nimeomba kibali kwa ajili ya kulima, nimeona kilimo hakinilipi, nikaamua niende nikafyatue matofali, nachangia nchi, najiongezea uchumi wangu, naongeza ustawi wa Taifa. Kosa liko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukubaliane, kubadili matumizi ya maji siyo kosa na huwezi kufungwa jela kwa sababu umebadili matumizi, tunarudi nyuma balada ya kwenda mbele. Unasema ni kosa mtu kutumia maji bila kibali; amesema vizuri kaka yangu pale Mheshimiwa Sanga, hivi mtu aliyeko kijijini kule Mwamalili, anachukua mifugo yake anapeleka mtoni kwa ajili ya kwenda kunywesha mifugo yake. Anajuaje hizi habari za kibali anazoziweka Waziri hapa? Ukiacha hivyo, aende akanyweshee wapi mifugo yake? Mheshimiwa Waziri, tengeneza miundombinu, weka mabwawa ya kunyweshea mifugo, weka mabwawa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji, weka center, husisha sekta binafsi wakusaidie. Kama mzigo ni mkubwa kwa ajili ya kuwahudumia watu, kuwapelekea maji na maji yenyewe yapo, hivi Serikali mngepewa kazi ya kutengeneza maji! Maji ni ya Mungu, maji yapo, kazi yenu ninyi ni kuyapeleka kwa wananchi. Mngepewa kazi ya kutengeneza haya maji jamani tungekuwa tunalipa shilingi ngapi? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji kama yapo, kazi ni ndogo tu. Kama unaona Serikali inatumia fedha nyingi kuwapelekea wananchi huduma ya maji, huduma bora, basi usiweke faini na vikwazo. Miaka zaidi ya 60 ya uhuru kweli tunaambiana hapa, “mtu akitumia maji kupita kiasi,” hivi mimi nitajuaje ng’ombe wangu anahitaji kunywa maji lita 20 na siyo lita 15? Nitajuaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusitunge sheria kama vile Tanzania nzima ni Dar es Salaam au kama vile Watanzania wote wanaishi mjini. Watu wanaishi vijijini. Umetanua hapa, umeweka hii sheria imeenda mpaka kwenye mabonde ya maji, sijui maji yanayoporomoka; hivi kweli wale watu wa kule watajua haya mambo yako unayosema hapa sijui kibali, ubadilishe matumizi!

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri akumbuke asilimia zaidi ya 80 ya Watanzania wanaishi vijijini.

MHE. ESTER BULAYA: Eeh!

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, maji haya ni ya Mungu, usiwawekee watu masharti ya kutumia maji. Ndiyo maana mwingine anaoga maji ndogo ya lita 20, mwingine anaoga maji ndoo ya lita 10.

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Usiweke vikwazo vya matumizi ya maji...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome subiri, kuna taarifa huku.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Alah!

MWENYEKITI: Mheshimiwa Eng. Mwanaisha.

TAARIFA

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba, maji ni ya Mungu lakini namna ya ku- utilize maji ni lazima yatengenezewe utaratibu, kwa sababu underground water resources ni mkondo ambao una-channels. Kama channel haitakuwa limited, ndiyo yanayotokea, visima vinachimbwa na maji yanakauka. Serikali inaingiza fedha nyingi humo, lakini matumizi yetu mabaya yanapelekea visima kukauka. Kwa hiyo, ni lazima kuwe na utaratibu wa kuzuia maji yale hata kama ni ya Mungu. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome Makamba, unaipokea hiyo taarifa!

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashukuru na bahati nzuri Bunge liko live, ndiyo bahati nzuri yake. Yaani ninyi mmeenda kwa wananchi kuomba kura, mkawaambia mtawapelekea maji, mkawaambia mtahikikisha wanapata maji ya kutosha, mnamtua mama ndoo kichwani, sasa hivi tunaweka sheria kwamba mtu atakayetumia maji kupita kiasi atatozwa faini ya Shilingi milioni 10 au atafungwa jela miezi sita.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa wapi? Mheshimiwa Salome subiri kidogo. Taarifa Mheshimiwa.

T A A R I F A

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa unyenyekevu sana naomba nimpe taarifa dada yangu Mheshimiwa Salome. Kwanza sheria tunayoifanyia mabadiliko siyo ya usambazaji wa huduma za maji, tunafanya mabadiliko ya sheria ya inayo-manage vyanzo vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, asijikite kwenye sheria ya usambazaji, hii ni sheria ya management ya vyanzo vya maji na ndiyo maana tunasema, kubadilisha matumizi ya maji ni lazima upewe kibali. Kile kibali maana yake ni nini? Tunakuwa tumefanya tathmini kuona kwa shughuli yako unahitaji maji kiasi gani? Ya namna gani? Unapotaka kubadilisha matumizi, utaomba kibali na sheria iko vizuri. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome naomba umalizie kwa nusu dakika.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri huyo pia ni Mbunge wa Jimbo. Kwa hiyo, watu wakiwa kwenye jimbo lake, wakitaka kutumia maji kunyweshea mifugo, yale maji ya mabondeni, yale maji ya mtoni, wanatakiwa wakaombe kibali cha kutumia maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ihakikishe watu wanapata maji, itengeneze miundombinu ya watu kupata maji, ihakikishe inatengeneza mabwawa kwa ajili ya umwagiliaji, kwa ajili ya kilimo, kwa ajili ya mifugo. Ihakikishe inawapelekea watu maji kwenye maeneo yao. Hakuna mtu anayependa kutoka kwake ateremshe bondeni kwenda kunywesha mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Sheria ya Maji naikubali. Changamoto yake ni kwamba inalenga kwenda kudhibiti badala ya kuboresha miundombinu ya maji kwa watu wetu. Kwa hiyo, ombi langu na rai kubwa kwa Serikali na nimeleta schedule of amendment. Kwanza, hizi faini ziondolewe. Ni mapema sana kuweka hizi faini kwa wananchi. Watu wataumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamesema hapa, hata haya yanayoandikwa humu hawayajui. Sisi tunajifanya tuna busara kubwa tunapochangia, lakini ukweli ni kwamba wanaoenda kutekeleza hii sheria watasimamia mkono wa chuma na watu wetu wataumia. Tufute haya masharti, watu waboreshewe miundombinu, na automatically tukiboresha miundombinu maji yatatumika vizuri, automatically tukiboresha miundombinu hakuna mtu ataenda mtoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani mimi nalima, kiangazi kimekuja ghafla, nahitaji kumwagilia eneo langu kwa maji kutoka mtoni, unaniambia lazima nikaombe kibali, mazao hayasubiri kibali. Nami sikujua kama mvua itakata ghafla. Kwa hiyo, ombi langu, kwa heshima na taadhima, hii sheria imekuja mapema sana. Hivyo vyanzo vya maji tunavyotaka kuvilinda, ni kweli, lakini hawa wananchi wanapata hiyo huduma ya maji? Ofisi ya Waziri wa Maji inatekeleza majukumu yake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejaribu tu ku-post picha hapa niko Bungeni nikasema leo tuna Muswada wa Maji, zimekuja comments kibao. Watu wanasema, hata hayo maji yenyewe ukienda kuomba uvutiwe nyumbani kwako ni shughuli. Watu wanaovuta maji wamekuwa mabosi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Muswada wa Sheria ya Tume ya Mipango wa Mwaka 2023.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nichangie Miswada hii mitatu ambayo imeletwa mbele ya Bunge letu leo tuweze kutoa maoni yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuipongeza Serikali kwa kuleta Muswada unaohusiana na Tume ya Mipango. Nina mambo mawili ninataka kushauri kuhusiana na Tume ya Mipango pamoja na uzuri wake na Muswada wake kuwa mzuri nina mambo mawili.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ni kuhusiana na kifungu cha tano cha Muswada ambacho kinasema “Mheshimiwa Rais ndiye atakuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mipango”. Ukisoma kifungu cha tano ambacho kina mruhusu Mheshimiwa Rais kuwa Mwenyekiti ukaenda kusoma kifungu cha saba cha Muswada pamoja na maneno mengine wanasema Tume hii ya Mipango ndio itakuwa chombo cha juu cha ushauri kinacho wajibika kwenye Baraza la Mawaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa ufahamu wangu mdogo Mheshimiwa Rais anaelekeza hawezi kushauri, akisema ni malekezo ni lazima yafanyike. Ukisema kwamba Tume ya Mipango ambayo Mheshimiwa Rais ndio alikuwa Mwenyekiti wakatengeneza mipango ndio inaenda kushauri kwenye Baraza la Mawaziri maana yake kila kitu lazima kifanyike. Kwa mantiki hiyo ni kwamba kama Tume ya Mipango kuna makosa au kuna mambo madogo ambayo yanatakiwa yafanyiwe marekebisho Baraza la Mawaziri litakosa mandate ya kuyarekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa minajiri hiyo, ninashauri kuweka kwenye Ofisi ya Mheshimiwa Rais ni jambo jema lakini tungetengeneza mamlaka kamili ambayo inakuwa na Kurugenzi zake ambayo kazi yao ni kutengeneza hiyo mipango watakuwa na wataalam na watamshauri Mheshimiwa Rais na hawa watakuwa kama ni timu ya wataalam ambao pia itakwenda kufanya mawasilisho kwenye Baraza la Mawaziri na kulishauri Baraza la Mawaziri. Kwa hiyo naungana kabisa na hoja ya Tume ya Mipango lakini kumuweka Mheshimiwa Rais kama Mwenyekiti naona kidogo inaleta ukakasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili ni kuhusiana namna hii Tume ya Mipango ilivyotengenezwa. Nashauri ili mipango iweze kupangwa vizuri kama walivyosema Wabunge wenzangu ni lazima sekta zote na wadau wote waweze kushirikishwa bado sijaona ushiriki wa Sekta Binafsi kwenye Tume hii ya Mipango na wote tunakubaliana kwamba mipango mingi inayotekelezwa mingi inahusisha Sekta Binafsi. Kwa hiyo, hilo ningetamani sana liweze kuzingatiwa katika Muswada huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine niende kwenye Sheria ya Usalama wa Taifa. Sheria ya Usalama wa Taifa imefanyiwa marekebisho lakini niseme tu mambo mengi ambayo yameletwa kwenye Sheria hii yanafanyika tayari huko mtaani. Kwa mfano wameweka kifungu kinachoruhusu wastaafu wa Usalama wa Taifa.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa inatoka wapi? Anhaa Mheshimiwa Gwajima, kwa sababu mpo Gwajima wawili inabidi nimtaje jina lote Mheshimiwa Askofu Josephat Gwajima.

TAARIFA

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, naam! Napenda tu kumpa taarifa mchangiaji, pamoja na mchango mzuri anaousema kwamba siyo vizuri Tume ya Mipango kuwa chini ya Uenyekiti wa Rais. Nataka nimjulishe kwamba mipango yote inahitaji political will na kwenye nchi zetu mahala ambapo Rais wa nchi pia ni Mwenyekiti wa Chama ni muhimu Mwenyekiti wa Chama na Rais wa nchi awe chairman wa hiyo Tume ya Mipango ili a-push Serikali na political will pia.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba unapokea taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, kwanza kikanuni ulituelekeza ukishaenda kwenye hoja nyingine mtu hawezi kukupa taarifa kwenye hoja uliyoimaliza lakini taarifa hiyo siipokei kwa mantiki ile niliyoisema Rais hashauri anaelekeza. kwa hiyo hiyo issue ya political will vivyo hivyo akiichukulia kwa upande hasi kwa upande chanya atasukuma lakini akiwa kwa upande hasi atazuia kwa hiyo, niseme Tume ya Mipango imshauri na iweze kuwajibishwa.

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Sheria ya Usalama wa Taifa. Nimesema hapa mambo mengi ambayo yameshauriwa kwenye Muswada huu tayari yanafanyika kwa mfano kuna kifungu cha saba nafikiri kinasema waweze kumiliki silaha, tayari wanamiliki silaha. Kifungu cha tano wanasema kuwalinda watu, sasa hapo ndio nataka niweke mkazo kidogo. Moja kati ya orodha ya watu ambao wanatakiwa kulindwa ni wagombea wa Urais wa vyama vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiisoma kama ilivyo kwenye Sheria unaona nia njema kabisa ya Serikali ukija kwenye utekelezaji huwezi kutofautisha taasisi hii na Serikali iliyoko madarakani, mfungamano wake ni mkubwa sana. Ni kweli kila mgombea Urais ili aweze Kushika dola ni lazima akubalike na vyombo vyote vya dola ili waweze kumpa dhamana ya kuongoza nchi.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai, najua tabia hufa polepole bado tuna changamoto kubwa ya Vyombo vyetu vya Usalama kutofautisha kati ya..

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, kuhusu taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro, Waziri wa Katiba na Sheria.

TAARIFA

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA; Mheshimiwa Spika, ahsante sana naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Salome Makamba kwamba mgombea Urais yoyote ni Potential President, anauwezo wa kuongoza nchi hii kesho na sisi tuna mchukulia sawa, wagombea wote hawa wana haki sawa. Kwa hiyo, ukimuacha pasipokuwa na ulinzi akadhuriwa kuna uwezekano wa kumuua Rais wa kesho. Lazima tumlinde leo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ulichokisema ndio nilichokisema kwa hiyo tuliza ball tuendelee hapa. Ulichokisema ndio nilichokisema mimi na hoja yangu ni kwamba watu wa vyombo hasa Usalama wa Taifa ni lazima wafahamu kwamba wao wanatakiwa kuwa impartial linapofikia kwenye suala la uchaguzi. Kazi yao ni kumlinda Mgombea Urais kwa maslahi ya Usalama wa Taifa na siyo usalama wa chama na hiyo ndiyo hoja yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kifungu ambacho kinasema Usalama wa Taifa hawatashitakiwa…

SPIKA: Mheshimiwa Salome ngoja nielewe jambo moja kutoka upande wa Serikali. Huu Uchaguzi wa 2020 Wagombea Urais wote walipewa walinzi wale walinzi wale waliokuwa nao wanatokea wapi? Annh! Sasa ndio sema kwenye kisemeo maana ukinijibu hivyo kitakuwa hakiingii kwenye Taarifa Rasmi za Bunge. Wale walinzi waliokuwa wamepewa 2020 na miaka mingine kuko nyuma wanatokea wapi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, walinzi wote walikuwa wanatokea Idara yetu ya Usalama wa Taifa.

SPIKA: Kwa hivyo ni sahihi kwamba Sheria hii hakuna jambo jipya inayoleta hicho ndicho kilichopo mpaka sasa hivi? Nitakuwa sahihi nikisema hivyo. (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nachelea sasa sijui tujibu wakati tunajumuisha

SPIKA: Wewe nijibu mimi nataka kuelewa ili nimalizane na hoja ya Mheshimiwa Salome.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, Sheria hii imeleta mambo yote ambayo yanatakiwa kufanyika kwa muktadha wa sasa kwa hiyo hata unavyoona kwa mfano kwenye hiyo orodha ya wale viongozi tunawapa ulinzi pia tumeongeza watu lakini pia tumetengeneza vizuri iweze ku-fit protocols kwa hiyo tunakwenda…

SPIKA: Nataka kuelewa tu hii ya Urais. Wanalindwa na watu wanotoka Idara ya Usalama wa Taifa?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, ndio wanalindwa na watu wanaotokea Idara ya Usalama wa Taifa.

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Salome Makamba, malizia mchango wako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante jambo lingine kwenye Sheria hiyo. Jambo ambalo limeanzishwa ni kwamba hawa Usalama wa Taifa hawatashtakiwa kwenye makosa ya kijinai ambayo watayafanya wakiwa wanatekeleza majukumu yao kwa nia njema.

Mheshimiwa Spika, nia njema sijui tunaipimaje, sijui tunaipimaje wakati huohuo wamepewa ruhusa ya kumiliki silaha, wakati huohuo Sheria hii hii inasema hawa watu hawatakiwi kufichuliwa yaani wakiwa mahali hawatakiwi kufichuliwa hii iko kwenye vifungu vya sheria hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni ngumu kuipima nia njema, nashauri Serikali tuliangalie vizuri jambo hili ili tuweze angalau tulinde maslahi ya vijana wetu ambao wanafanya kazi kwenye idara hii, kazi ngumu na ya hatari lakini pia tulinde maslahi ya Watanzania ambao kuna wakati wanashindwa kukwepana na mazingira hayo, tulinde maslahi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nitakwenda kwenye Sheria ya Usimamizi na Tozo za Ushuru wa Bidhaa, Mheshimiwa Waziri amesema wamebadilisha Kifungu cha 100 kwenye sheria hii kwenye Sheria ya Urekebu. Wamebadilisha Kifungu cha 100 kwa kuelekeza fedha zote zinazopatikana kutokana na Serikali kushinda kesi za za kikodi zipelekwe Hazina. Hizi fedha, sheria iko tangu 2006 ikafanyiwa marekebisho 2008 na fedha hizi zilikua zinatakiwa ziende kwenye mfuko; nataka kuhoji Mheshimiwa Waziri hizi fedha zilikua zinaenda wapi? Ni shilingi ngapi? Tutazipataje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nishauri tu tufanye special audit kwenye eneo hili, kwasababu Serikali imeshinda kesi nyingi za kikodi na fedha zile zimerudishwa. Tumeona hapa kuna mambo ya kina plea bargaining billions money zilikua zinarudishwa Serikalini, zimekwenda wapi? Zilitakiwa ziende kwenye mfuko since 2006, 2008 sasa hivi wanasema ziende Hazina, je, na zile ambazo zimefanyika huko nyuma kabla ya kuwepo kwa sheria hii na zenyewe zitapelekwa Hazina? au … (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Yatokanayo na Urekebu wa Sheria wa Mwaka 2023 .
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nichangie Miswada hii mitatu ambayo imeletwa mbele ya Bunge letu leo tuweze kutoa maoni yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuipongeza Serikali kwa kuleta Muswada unaohusiana na Tume ya Mipango. Nina mambo mawili ninataka kushauri kuhusiana na Tume ya Mipango pamoja na uzuri wake na Muswada wake kuwa mzuri nina mambo mawili.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ni kuhusiana na kifungu cha tano cha Muswada ambacho kinasema “Mheshimiwa Rais ndiye atakuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mipango”. Ukisoma kifungu cha tano ambacho kina mruhusu Mheshimiwa Rais kuwa Mwenyekiti ukaenda kusoma kifungu cha saba cha Muswada pamoja na maneno mengine wanasema Tume hii ya Mipango ndio itakuwa chombo cha juu cha ushauri kinacho wajibika kwenye Baraza la Mawaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa ufahamu wangu mdogo Mheshimiwa Rais anaelekeza hawezi kushauri, akisema ni malekezo ni lazima yafanyike. Ukisema kwamba Tume ya Mipango ambayo Mheshimiwa Rais ndio alikuwa Mwenyekiti wakatengeneza mipango ndio inaenda kushauri kwenye Baraza la Mawaziri maana yake kila kitu lazima kifanyike. Kwa mantiki hiyo ni kwamba kama Tume ya Mipango kuna makosa au kuna mambo madogo ambayo yanatakiwa yafanyiwe marekebisho Baraza la Mawaziri litakosa mandate ya kuyarekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa minajiri hiyo, ninashauri kuweka kwenye Ofisi ya Mheshimiwa Rais ni jambo jema lakini tungetengeneza mamlaka kamili ambayo inakuwa na Kurugenzi zake ambayo kazi yao ni kutengeneza hiyo mipango watakuwa na wataalam na watamshauri Mheshimiwa Rais na hawa watakuwa kama ni timu ya wataalam ambao pia itakwenda kufanya mawasilisho kwenye Baraza la Mawaziri na kulishauri Baraza la Mawaziri. Kwa hiyo naungana kabisa na hoja ya Tume ya Mipango lakini kumuweka Mheshimiwa Rais kama Mwenyekiti naona kidogo inaleta ukakasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili ni kuhusiana namna hii Tume ya Mipango ilivyotengenezwa. Nashauri ili mipango iweze kupangwa vizuri kama walivyosema Wabunge wenzangu ni lazima sekta zote na wadau wote waweze kushirikishwa bado sijaona ushiriki wa Sekta Binafsi kwenye Tume hii ya Mipango na wote tunakubaliana kwamba mipango mingi inayotekelezwa mingi inahusisha Sekta Binafsi. Kwa hiyo, hilo ningetamani sana liweze kuzingatiwa katika Muswada huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine niende kwenye Sheria ya Usalama wa Taifa. Sheria ya Usalama wa Taifa imefanyiwa marekebisho lakini niseme tu mambo mengi ambayo yameletwa kwenye Sheria hii yanafanyika tayari huko mtaani. Kwa mfano wameweka kifungu kinachoruhusu wastaafu wa Usalama wa Taifa.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa inatoka wapi? Anhaa Mheshimiwa Gwajima, kwa sababu mpo Gwajima wawili inabidi nimtaje jina lote Mheshimiwa Askofu Josephat Gwajima.

TAARIFA

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, naam! Napenda tu kumpa taarifa mchangiaji, pamoja na mchango mzuri anaousema kwamba siyo vizuri Tume ya Mipango kuwa chini ya Uenyekiti wa Rais. Nataka nimjulishe kwamba mipango yote inahitaji political will na kwenye nchi zetu mahala ambapo Rais wa nchi pia ni Mwenyekiti wa Chama ni muhimu Mwenyekiti wa Chama na Rais wa nchi awe chairman wa hiyo Tume ya Mipango ili a-push Serikali na political will pia.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba unapokea taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, kwanza kikanuni ulituelekeza ukishaenda kwenye hoja nyingine mtu hawezi kukupa taarifa kwenye hoja uliyoimaliza lakini taarifa hiyo siipokei kwa mantiki ile niliyoisema Rais hashauri anaelekeza. kwa hiyo hiyo issue ya political will vivyo hivyo akiichukulia kwa upande hasi kwa upande chanya atasukuma lakini akiwa kwa upande hasi atazuia kwa hiyo, niseme Tume ya Mipango imshauri na iweze kuwajibishwa.

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Sheria ya Usalama wa Taifa. Nimesema hapa mambo mengi ambayo yameshauriwa kwenye Muswada huu tayari yanafanyika kwa mfano kuna kifungu cha saba nafikiri kinasema waweze kumiliki silaha, tayari wanamiliki silaha. Kifungu cha tano wanasema kuwalinda watu, sasa hapo ndio nataka niweke mkazo kidogo. Moja kati ya orodha ya watu ambao wanatakiwa kulindwa ni wagombea wa Urais wa vyama vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiisoma kama ilivyo kwenye Sheria unaona nia njema kabisa ya Serikali ukija kwenye utekelezaji huwezi kutofautisha taasisi hii na Serikali iliyoko madarakani, mfungamano wake ni mkubwa sana. Ni kweli kila mgombea Urais ili aweze Kushika dola ni lazima akubalike na vyombo vyote vya dola ili waweze kumpa dhamana ya kuongoza nchi.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai, najua tabia hufa polepole bado tuna changamoto kubwa ya Vyombo vyetu vya Usalama kutofautisha kati ya..

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, kuhusu taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro, Waziri wa Katiba na Sheria.

TAARIFA

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA; Mheshimiwa Spika, ahsante sana naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Salome Makamba kwamba mgombea Urais yoyote ni Potential President, anauwezo wa kuongoza nchi hii kesho na sisi tuna mchukulia sawa, wagombea wote hawa wana haki sawa. Kwa hiyo, ukimuacha pasipokuwa na ulinzi akadhuriwa kuna uwezekano wa kumuua Rais wa kesho. Lazima tumlinde leo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ulichokisema ndio nilichokisema kwa hiyo tuliza ball tuendelee hapa. Ulichokisema ndio nilichokisema mimi na hoja yangu ni kwamba watu wa vyombo hasa Usalama wa Taifa ni lazima wafahamu kwamba wao wanatakiwa kuwa impartial linapofikia kwenye suala la uchaguzi. Kazi yao ni kumlinda Mgombea Urais kwa maslahi ya Usalama wa Taifa na siyo usalama wa chama na hiyo ndiyo hoja yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kifungu ambacho kinasema Usalama wa Taifa hawatashitakiwa…

SPIKA: Mheshimiwa Salome ngoja nielewe jambo moja kutoka upande wa Serikali. Huu Uchaguzi wa 2020 Wagombea Urais wote walipewa walinzi wale walinzi wale waliokuwa nao wanatokea wapi? Annh! Sasa ndio sema kwenye kisemeo maana ukinijibu hivyo kitakuwa hakiingii kwenye Taarifa Rasmi za Bunge. Wale walinzi waliokuwa wamepewa 2020 na miaka mingine kuko nyuma wanatokea wapi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, walinzi wote walikuwa wanatokea Idara yetu ya Usalama wa Taifa.

SPIKA: Kwa hivyo ni sahihi kwamba Sheria hii hakuna jambo jipya inayoleta hicho ndicho kilichopo mpaka sasa hivi? Nitakuwa sahihi nikisema hivyo. (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nachelea sasa sijui tujibu wakati tunajumuisha

SPIKA: Wewe nijibu mimi nataka kuelewa ili nimalizane na hoja ya Mheshimiwa Salome.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, Sheria hii imeleta mambo yote ambayo yanatakiwa kufanyika kwa muktadha wa sasa kwa hiyo hata unavyoona kwa mfano kwenye hiyo orodha ya wale viongozi tunawapa ulinzi pia tumeongeza watu lakini pia tumetengeneza vizuri iweze ku-fit protocols kwa hiyo tunakwenda…

SPIKA: Nataka kuelewa tu hii ya Urais. Wanalindwa na watu wanotoka Idara ya Usalama wa Taifa?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, ndio wanalindwa na watu wanaotokea Idara ya Usalama wa Taifa.

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Salome Makamba, malizia mchango wako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante jambo lingine kwenye Sheria hiyo. Jambo ambalo limeanzishwa ni kwamba hawa Usalama wa Taifa hawatashtakiwa kwenye makosa ya kijinai ambayo watayafanya wakiwa wanatekeleza majukumu yao kwa nia njema.

Mheshimiwa Spika, nia njema sijui tunaipimaje, sijui tunaipimaje wakati huohuo wamepewa ruhusa ya kumiliki silaha, wakati huohuo Sheria hii hii inasema hawa watu hawatakiwi kufichuliwa yaani wakiwa mahali hawatakiwi kufichuliwa hii iko kwenye vifungu vya sheria hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni ngumu kuipima nia njema, nashauri Serikali tuliangalie vizuri jambo hili ili tuweze angalau tulinde maslahi ya vijana wetu ambao wanafanya kazi kwenye idara hii, kazi ngumu na ya hatari lakini pia tulinde maslahi ya Watanzania ambao kuna wakati wanashindwa kukwepana na mazingira hayo, tulinde maslahi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nitakwenda kwenye Sheria ya Usimamizi na Tozo za Ushuru wa Bidhaa, Mheshimiwa Waziri amesema wamebadilisha Kifungu cha 100 kwenye sheria hii kwenye Sheria ya Urekebu. Wamebadilisha Kifungu cha 100 kwa kuelekeza fedha zote zinazopatikana kutokana na Serikali kushinda kesi za za kikodi zipelekwe Hazina. Hizi fedha, sheria iko tangu 2006 ikafanyiwa marekebisho 2008 na fedha hizi zilikua zinatakiwa ziende kwenye mfuko; nataka kuhoji Mheshimiwa Waziri hizi fedha zilikua zinaenda wapi? Ni shilingi ngapi? Tutazipataje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nishauri tu tufanye special audit kwenye eneo hili, kwasababu Serikali imeshinda kesi nyingi za kikodi na fedha zile zimerudishwa. Tumeona hapa kuna mambo ya kina plea bargaining billions money zilikua zinarudishwa Serikalini, zimekwenda wapi? Zilitakiwa ziende kwenye mfuko since 2006, 2008 sasa hivi wanasema ziende Hazina, je, na zile ambazo zimefanyika huko nyuma kabla ya kuwepo kwa sheria hii na zenyewe zitapelekwa Hazina? au … (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuwawakilisha wananchi wangu wa Shinyanga katika bajeti hii ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyeki, napenda kuongea na Mheshimiwa Waziri na kumwomba atusaidie matatizo ya ushirika pale Kahama. Mheshimiwa Waziri wote tunafahamu Sheria ya Ushirika namba 20 ya mwaka 2003 inasema wazi kwamba Ushirika ukifilisika mali zake zitakwenda katika Ushirika mwingine. Hilo limekuwa likifanyika tangu mwaka 1984, mwaka 1986, lakini cha kushangaza hivi karibuni pale Kahama Chama cha Ushirika kimepewa Kampuni. Wamepewa Kampuni kinyume na utaratibu na Mahakama imetengua lakini mpaka leo Chama kile cha Ushirika
kimeng’ang’aniwa na Kampuni na wale wananchi ambao walijiunga pamoja, ambao ni wakulima wadogo wadogo wakatengeneza Ushirika, wakajenga vibanda, wamenyang’anywa maeneo yao. Suala hili nimeshalipigia kelele mara nyingi humu Bungeni na hakuna msaada wowote unaoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri alitazame jambo hili kwa jicho la pekee. Wale wakulima ni watu ambao ni wanyonge, hawana pesa, hawawajui watu wakubwa, lakini kwa sababu walioko pale ni mapapa, ni mafisadi, wamewanyang’anya maeneo yao wale watu, vibanda zaidi ya 200 vimechukuliwa, soko lile limemilikishwa kwa mtu mmoja ambaye ndiye mwenye hisa nyingi kwenye Kampuni ile na wale watu wanakosa pa kukimbilia. Namfahamu vizuri Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Tizeba ni mtetezi wa wanyonge. Namwomba sana aje kwetu pale atusaidie kutatua tatizo hili kwa sababu limekuwa ni tatizo sugu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi wale watu wakihoji kuhusu Ushirika Mheshimiwa Waziri wanakamatwa, wanaenda kuwekwa ndani, wanaanza kuhojiwa, wanatishwa, vitisho hivyo ni unyanyasaji kwa raia wanyonge wa Tanzania hii. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie kutatua tatizo la ushirika kwa sababu limezidi, kwanza ni kinyume cha Sheria, Mahakama imeshatengua Kampuni ile kumiliki, ile hati iliyopo pale ya Kampuni imetenguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza wanatakatisha hati ile, wanafanya kui-renew ili ionekane kwamba ni hati halali. Kweli tatizo hili limezidi, limekuwa la muda mrefu lina miaka zaidi ya 27, tunaomba Mheshimiwa Waziri tafadhali aje atusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka hapo niongelee suala la upigaji chapa ng’ombe, tumezinduliwa mradi sasa hivi wa kupiga chapa ng’ombe. Wanasema ni kwa ajili ya sababu za kiusalama wanataka kutambua ng’ombe na wale wanaokuja kutoka nchi za jirani. Hata hivyo, wanasema upigaji chapa hawa ng’ombe gharama yake ni Sh.3,000/= kwa kila ng’ombe. Sisi Wasukuma tunasifika kwa ufugaji. Familia za vijijini Sh.3000/=, Sh.1,000/= ya kula tunahangaika kutafuta hiyo Sh.3,000/= tutaitoa wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ndizo tozo za kero ambazo zilipigwa marufuku na Mheshimiwa Magufuli. Kama wanaleta mradi basi watafute namna ya kuutekeleza mradi ule bila kuwaumiza wananchi na Mheshimiwa Waziri anafahamu kabisa kwamba kupiga chapa ng’ombe kunashusha thamani ya ngozi ile inapotakiwa kuuzwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunasema tunakwenda kwenye Tanzania ya Viwanda, tunasema tuwakwamue wananchi kwenye umaskini, leo tunaenda kuwapiga chapa ng’ombe wao na tunawatoza Sh.3,000/=. Tunaomba majibu tunahitaji kujua ni njia gani itatumika kuwapiga chapa bila kuwabughudhi, bila kuwakera wakulima hawa ambao ufugaji kwao ni biashara, ufugaji ni maisha, lakini ufugaji kwao ndiyo chakula cha kila siku na ndio utamaduni wetu vile vile. Tunaomba Mheshimiwa Waziri atusaidie sana majibu juu ya hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee pia suala la punda. Usukumani punda wanatumika kwa ajili ya kubeba mizigo, maji, ndio usafiri kule kwetu. Hata hivyo, hivi leo nikikueleza punda wanauawa, punda wanauzwa, wamekuwa ndio biashara. Mheshimiwa Waziri, China wanabiashara ya ngozi, wananunua ngozi hizi za punda na wanatengeneza anti aging, dawa ambayo inayozuia kuzeeka na inaongeza nguvu za kiume pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa ya Mheshimiwa Waziri, biashara hii…

MWENYEKITI: Mheshimiwa umesemaje? (Kicheko)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la punda lina dawa ambayo inatumika kule China kupunguza kuzeeka, lakini pia inaongeza nguvu za kiume. Kwa sababu hiyo thamani ya punda ni Sh.50,000/= mpaka Sh.190,000/=, lakini thamani ya ngozi ya punda ni pound 160, ngozi peke yake. Juzi Mheshimiwa Mwijage wakati anapitisha bajeti yake hapa alisema amepiga marufuku uuzaji wa punda. Hii haitoshi, tunatakiwa tuisimamie kama tunavyopiga marufuku mambo ya pembe za ndovu na biashara nyingine, kwa sababu hii itapelekea kupotea kwa hawa punda ambao ni mifugo tunayoitegemea sisi kama njia ya usafirishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tumeamua kuingia kwenye biashara hiyo basi tuwe na mechanism ya kuongeza hawa punda wawepo wawe ni wanyama wa biashara, waongezeke tuwe na jinsi ya kuboresha, kwa sababu hii mifugo iko chini ya Wizara yako na hii mifugo sisi tunaitumia kama njia ya usafirishaji kule kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ethiopia wana mifugo milioni 7.5 hii ya aina ya punda, lakini kuna nchi ambazo zimepiga marufuku na wameweka sheria, nchi kama Burkina Faso, Niger na Pakistan wameshaweka Sheria. Kusema tu haitoshi, tunafungua mianya ya wale watu ambao watakuwa wanafanya ujangili wa mifugo hii. Tusifungue mianya kwa sababu hatimaye itatuathiri sisi wenyewe. Tuweke sheria ambazo zitazuia, lakini kama unataka kufanya biashara hiyo na wafanye kwa njia halali na kuwe na misingi ya kuzuia upotevu wa wanyama hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu kwa kweli Ushetu, Tarafa ya Mweli hakuna hata josho, tarafa nzima ina kata karibu sijui ngapi, hakuna hata josho la kuoshea ng’ombe. Sasa bajeti ya Kilimo na Mifugo haifiki hata trilioni moja na tunategemea eti huu uti wa mgongo wa Kilimo Kwanza; sijui hata hiyo sera iliishia wapi; tunategemea eti malighafi itokane na mazao wa kilimo na mifugo, eti uti wa mgongo wa nchi hii ni kilimo, wakati huo huo hata bajeti yenyewe haiakisi malengo ya nchi hii ya Tanzania ya kutokana na malighafi za kilimo na mifugo. Hivi kwa nini tuendelee kuwadanganya Watanzania? Mimi sina wasiwasi na ukusanyaji wa kodi katika nchi hii, wasiwasi wangu ni allocation ya bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri atueleze mkakati wake wa kuongeza kilimo na mifugo kwa nchi hii kuelekea ku-connect na wazo la Tanzania ya viwanda ukoje? Ukiangalia ni theory tu, utekelezaji wa theory hii mimi siuoni, naona tu ni maneno yanasemwa na mwakani wanatumia kitabu kile kile wanabadilisha mwaka wanabadilisha vitu vidogo wanarudisha kitu kile kile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atusaidie, anaakisi vipi, anashirikiana vipi na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kutengeneza barabara ili atusaidie kule Ushetu, Kinamapula, Nyandele sijui Wandele sijui wapi, anatusaidia vipi kuleta barabara tuweze kulima kilimo cha tumbaku? Pamba imeshakufa, zao la biashara tulilonalo Shinyanga sasa hivi ambalo tunalitegemea ni tumbaku, lakini hakuna miundombinu iliyoboreshwa kila siku ni hadithi mtatekeleza lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nami niweze kuchangia bajeti hii japo kwa dakika tano. Nimesoma vizuri kitabu cha Mheshimiwa Waziri. Jambo kubwa lililopelekea tukashindwa kufanikisha bajeti iliyopita ni ukosefu wa fedha za wahisani. Kukosa fedha za wahisani Mheshimiwa Waziri anasema eti tulichelewa kufanya negotiation na wahisani ndiyo maana tulichelewa kupata pesa.

Mheshimiwa Waziri, wahisani wanatupa pesa pale tutakapokuwa tumetimiza masharti ya kupewa mikopo. Hatuwezi kupewa pesa kama Serikali yetu haizingatii utawala wa kidemokrasia, haizingatii utawala bora, uhuru wa vyombo vya habari na tunapitisha Sheria kandamizi zinazowakandamiza Watanzania. Mheshimiwa Waziri angekuwa mkweli juu ya hilo, kwamba tunahitaji tusimamie utawala bora, utawala wa sheria na kila mtu awe chini ya sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anasema kwenye kitabu chake, ili tuweze kupunguza deni la Taifa, ameamua kuwekeza miundombinu kwenye maeneo ambayo yanachochea uchumi. Miundombinu hiyo anataja ni barabara, reli na ndege. Bajeti inapitishwa tunakwenda kujenga kiwanja cha ndege Chato; hivi kweli Tanzania nzima tukitafuta sehemu zenye vichocheo vya kiuchumi utataja Chato kweli? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chato wameweka traffic light!

Inapita gari moja baada ya saa nzima ndiyo inapita gari pale. Wanaweka kiwanja cha ndege wanasema pale ndiyo kuna vichocheo, tupate pesa kwa ajili ya kuboresha uchumi kwenda kulipa deni la Taifa. Hizi ni ndoto ambazo haziwezi kutekelezeka. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeweka Sh.40/= kwenye mafuta ikiwa ni mbadala wa Motor Vehicle Licence. Kweli mafuta ya taa wataalam wetu waliosomeshwa na pesa za nchi hii wanasema tupandishe mafuta ya taa kwa sababu petroli imepanda, kwa sababu ndiyo njia pekee ya kuzuia uchakachuaji magari yasiharibike. Huo ndiyo utaalam wa Wazalendo wa Tanzania waliowekwa kwamba tuwakandamize masikini kuokoa magari yasiharibiwe, mafuta yatachakachuliwa. Huo ndiyo utaalam umeishia hapo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli sijaelewa vizuri kuhusu taratibu za manunuzi na Mheshimiwa Waziri wa Fedha anapokuja atueleze; kweli bado tunazingatia Sheria ya Manunuzi Tanzania au ni mtu mmoja ndio anaamua tununue vipi, tufanye vipi shughuli za manunuzi Tanzania?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba akija aje atueleze ni taratibu ipi ya manunuzi ilitumika kuwapa mkataba watu wanaokuja kujenga reli ya Dar es Salaam – Morogoro? Atueleze utaratibu upi ulitumika kununua zile ndege mbili ambazo mpaka sasa hivi inasemekana ndege moja iko down? Utaratibu upi ulitumika wa manunuzi kujenga barabara kwa pesa za uhuru barabara ya Mwenge – Morocco? Ni utaratibu upi umetumika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ndiyo mambo tulitegemea kuyaona kwenye bajeti hii ambayo sisi tulipitisha hapa sheria, watu wanakwenda kinyume na sheria, Bunge linadharauliwa kile tulichokifanya, halafu tumebaki tunacheka, tunapiga makofi, tunapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi bado sijapata picha ya zile propaganda zinazoenezwa kuhusu suala la madini na migodi. Tunaonekana kwamba sisi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi niweze kuchangia. Mwaka jana tulipitisha bajeti na tukakubaliana kwamba ili tuelekee Serikali ya viwanda, Tanzania ya viwanda, kuna baadhi ya maeneo ni lazima tuyaboreshe. Tukasema tutaboresha reli, tukasema tutaboresha barabara, bandari na maeneo mengi yenye vichocheo vya uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Kamati inaonesha kwenye ukurasa wa nne, Serikali haijapeleka bilioni 14 ambazo zilipitishwa kwa ajili ya sekta ya mawasiliano, haijapeleka bilioni sita ambazo tulipitisha kwa ajili ya kuboresha bandari ya Mwanza, hawajapeleka hata senti tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haijalipa Wakandarasi jambo ambalo limetuingiza kwenye deni la riba ya 3.9 bilioni, pesa hii tulipitisha lakini hazijapelekwa. Leo ni 2018 Watanzania wanaaminishwa tunakwenda kwenye Serikali ya Viwanda ilhali vichocheo ambavyo vinaweza kwenda kuhudumia viwanda kwa kusafirisha malighafi, kwa kuongeza utaalam mpaka leo havijapelekewa senti tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipitisha hapa bilioni mbili ikiwa ni pesa kwa ajili ya feasibility study ya uwanja wa ndege wa Chato, feasibility study, lakini leo tunaongea Bunge hili halikukaa halikupitisha popote uwanja wa ndege wa Chato umepelekewa bilioni 42 na completion stage ya project ya uwanja wa ndege wa chato ni zaidi ya asilimia 62, ilipitishwa wapi Bunge halikukaa, hatukuridhia, hakuna utaratibu wowote wa Serikali wa kimanunuzi ambao ulifanyika kupitisha ujenzi wa kiwanja hiki, leo tunacheka tu hapa na Serikali. Serikali inadharau Bunge, hakuna heshima kwa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, CAG anasema asilimia 35 ya maoni yake aliyoyatoa katika ripoti yake mwaka jana haijafanyiwa kazi, Serikali imepuuza na wala hawaoni umuhimu wa kufanya hivyo, iko kwenye ripoti ya CAG. Bunge linalalamika asilimia kubwa ya bajeti yake iliyopitishwa humu Bungeni haijatekelezwa leo tunakaa hapa tunasema tunakaa kuishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulizungumza hapa habari ya TARURA, tukasema tatizo la barabara za Wilaya sio chombo cha kutengeneza barabara, changamoto ni pesa katika maeneo haya. TARURA leo inatengewa asilimia 30, TANROAD inapewa asilimia 70, matokeo yake ni nini? Matokeo yake imeshindwa ku-perform kufanya kazi kwa sababu hawajapelekewa pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kahama ninakotoka mimi hakuna barabara inayopitika sasa hivi, ni mafuriko kila mahali, kwa sababu barabara zimeshashindwa kufanyiwa maintenance, pesa Serikali inapelekea inapotaka, halafu wanakuja hapa wanajifanya kichwa chini mikono nyuma, eti tuwape bajeti tuwapitishie, hakuna wanachokwenda kufanya ambacho tunashauri hapa Bungeni, wanatekeleza mambo yao wanayoyajua wao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mawaziri hawa ni Mawaziri welevu sana, yaani mimi leo ningekuwa ni hawa Mawaziri ningeomba nipumzike, kwa sababu hakuna wanachofanya pale ofisini zaidi ya kutekeleza miradi ya kuletewa na sio miradi ambayo inatokana na michango ya wananchi kupitia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwa sababu tu, sio kwamba hakuna makusanyo, kwa sababu pesa haziendi kwenye miradi. Wanawalazimisha wataalam wetu watafute njia mbadala ya kupata pesa.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kabla sijaanza kuchangia, naomba Bunge hili lijue mimi ni mjumbe wako wa Kamati ya Kanuni za Bunge na wewe kama Mwenyekiti wangu umenifundisha kweli kweli kuzisoma kanuni hizi na kuzizingatia. Kwa taarifa hiyo, naomba niwakumbushe Wabunge wenzangu kwamba tutumie tu lugha nzuri pale tunapokuwa tunachangia na tusiseme uongo Bungeni, tunamlazimisha Mheshimiwa Spika wakati mwingine kutubeba lakini si jukumu lake, tuwe na busara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kutoa quotation ya Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia Hassan Suluhu alipokuwa akiutubia katika sherehe za utoaji za tuzo za heshima, wakati ule alikuwa ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano. Mama Samia Suluhu alisema yafuatayo, imeandikwa kwa Kiingereza tafsiri nitakayoitoa haitakuwa ya moja kwa moja lakini alisema; “On the bilateral front the European Union is Tanzania key development partner both in terms of magnitude and financial support”.

Akaendelea kusema zaidi; “Let me therefore avail this opportunity to express our sincere gratitude and appreciation for the European Union in valuable assistance which has enabled the Government of Tanzania in many ways undertakes social economic development programs for sustainable development”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wajomba zangu kama Mheshimiwa Mzee Musukuma, Mama Samia Hassan Suluhu wakati anahutubia mkutano huu...(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuwa anamaanisha kwamba anatambua mchango mkubwa wa wadau wa maendeleo ambao wanatuchangia na bajeti yetu ya Tanzania. Mama Samia Hassan Suluhu ambaye sasa ni Vice President alitambua kabisa kwamba ili tuweze kutengeneza mpango wa maendeleo unaotekelezeka Tanzania haiwezi kujiendesha kwa pato la ndani peke yake.

T A A R I F A . . .

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyoniita Salome ameniita kwa Kisukuma, ni mjomba wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mama Samia Hassan Suluhu, nikianza kwa kum-quote alitambua mchango mkubwa wa wadau wa maendeleo kwenye bajeti yetu akiamini kwamba ili tuweze kufikia malengo ya mipango tunayoitengeneza ni lazima tuheshimu na tuthamini wadau wakubwa wa maendeleo katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ilivyo hivi sasa katika nchi yetu, mimi naomba nisisitize, kuna hali ya sintofahamu kubwa sana kati ya mahusiano yetu na wadau wetu wa maendeleo. Labda nianze na ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara kama tulivyoahidiwa wataishi kama mashetani wanaishi kama mashetani. Wafanyabiashara hawana security. Juzi tumeshuhudia billionaire mdogo Afrika ametekwa, amejirusha mwenyewe, halafu ameenda kuhojiwa akiwa nyumbani kwake na Serikali ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu pale Shinyanga tunao wafanyabishara wa maduka ya kati. Siku za hivi karibuni kwenye vyombo vya habari, Waheshimiwa Wabunge wenzangu mlishuhudia, Mkuu wa Mkoa amekwenda pale anafanya operesheni sijui ya ukaguzi, maana operesheni zimeshakuwa nyingi siku kila mtu anafanya; kwenye operesheni ile amefunga kwanza maduka yote ya pale mjini bila kujali athari za kiuchumi za matendo ambayo anayafanya. Kafunga maduka yale, kawachukua wafanyabiasha kaita vyombo vyote vya habari, anawasimamisha mbele ya vyombo vya habari anawaambia wafanyabiashara wale eleza ulichokifanya, haya kiri kwamba ulifanya hivi, haya eleza hivi, kinyume na haki za binadamu, utu, sera ya biashara na sera ya uwekezaji. Ndipo tulipofika kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, korosho na kahawa zinakufa. Mazao yote ya biashara ambayo kimsingi kama walivyoeleza Wabunge wenzangu ndiyo yanayochangia kwa kiasi kikubwa tuweze kutekeleza mpango huu ambao leo tumekaa Dodoma tunaujadili yanakufa lakini nobody cares. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikupe taarifa iliyotokea jana. Jana kwenye Citizen TV kwa Wabunge wenzangu ambao mmetazama, wavuvi 36 wa Kenya wamezuiliwa kwenye Ziwa Victoria wakisemekana kwamba ni wavuvi haramu na wamekatwa na watu wa Usalama wanaambiwa hawawezi kuachiwa mpaka walipe faini ya milioni 26. Je, watu wa Usalama wanatoza faini? Uvuvi haramu mamlaka husika zinajulikana lakini sasa ndipo tulipofika leo, tunasema refa wewe, mchezaji wewe, mfunga goli wewe, mtu mmoja anafaya kila kitu na niliwahi kusema humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetoka kusema asubuhi habari ya watu ambao ni watetezi wa waandishi wa habari Tanzania. Kuna sintofahamu kubwa, watu wamekuwa detained hotelini wamenyang’anywa passport.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema leo Serikali itoe kauli kukemea vitendo hivi ambavyo vinaweza kutuingiza kwenye migogoro ya kidiplamasia, hatuelewani humu ndani. Mpaka natamani neno diplomasia lingetafutiwa neno lingine labda ni msamiati mgumu ambao viongozi wa Serikali hawaelewi. Wale watu wamekuwa detained BBC na CNN wame-report. Hivi inaleta image gani kwa nchi yangu leo kudhalilika namna hiyo kimataifa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri Mahiga alitoa statement baada ya Balozi wa EU kuondoka, akasema eti ameondoka kwa anavyojua mwenyewe, amepangiwa kazi nyingine sisi hatuwezi kujua. Hata hivyo, Balozi wa EU ametoa statement kwenye tovuti yake, anasema kuwa alifanya na mazungumzo na Serikali ya Tanzania na akaeleza grievances zake kwamba Tanzania hawaelewani na EU kwa sababu kuna uvunjifu mkubwa haki za bidanamu, Tanzania kuna shida kubwa ya utawala wa sheria, ameeleza black and white. Alikuja akafanya mazungumzo mpaka anaondoka nobody cares. Serikali, Waziri mkongwe mdiplomasia ninayemuamini anatoka public anasema ameenda kupangiwa kazi nyingine mimi sijui bwana, inawezekana tukaletewa mtu mwingine, recalling of an Ambassador is not a joke ,naharibu image ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasimama leo hapa kutaka kukuonyesha kwamba hawa European Union inachangia…

T A A R I F A . . .

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwakumbushe Watanzania wenzangu kwamba leo tunapozungumza hapa ndani kwenye kwa Taarifa ya Hali ya Uchumi ya mwaka huu 2018, European Union yenye nchi 27,28 imechangia kwenye kahawa dola milioni 149.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru nichangie Wizara hii muhimu na Wizara ambayo imepelekewa fedha nyingi kuliko Wizara zote katika Serikali hii ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa baraka aliyotujalia ya kuweza kupatikana kwa ndugu yetu bwana Mdude Nyangari. Akiwa hai japo amejeruhiwa vibaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja kabla sijaanza kuchangia, jana ilizunguka taarifa ambayo inasemekana imetoka Ikulu, ikionyesha kwamba Mheshimiwa Rais anasikitishwa sana na vitendo vya utekaji na upoteaji wa watu vinavyoendelea katika nchi hii, na akasema kwamba vitendo hivi vinaichafua nchi na ameliagiza jeshi la polisi kufanyia kazi na ataunda tume na ikibidi…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Makamba jielekeze kwenye hoja, ambayo ko mbele yako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naenda kwenye hoja. Ghafla bini vuu tukapata taarifa kutoka Ikulu ikikanusha habari hiyo…

MWENYEKITI: Makamba, jielekeze kwenye hoja ambayo iko mbele yako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kukanusha taarifa inayotoka Ikulu ni taarifa nzuri sana…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Makamba nitakukalisha sasa hivi, jielekeze kwenye hoja ambayo ipo, kwa mujibu wa kanuni, jielekeze kwenye hoja ambayo iko mbele yako.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wa Nchi yetu amefanya kazi kubwa sana katika kusimamia Wizara ya Uchukuzi na Mawasiliano, na mtizamo wake Mheshimiwa Rais, katika kusimamia suala la ununuzi wa ndege, Mheshimiwa Rais amehamishia Mamlaka ya Usimamizi wa Ndege zote za Serikali katika Ofisi ya Rais. Jambo hili, katika miradi mikubwa katika nchi hii, katika miradi mikubwa, mradi wa ndege ni mmoja kati ya miradi mitatu mikubwa iliyoanzishwa katika hii nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vote 20, haikaguliwi na Mkaguzi Mkuu wa Serikali. Fedha za wananchi ambazo ndizo nyingi zinatumika katika mradi huu, zimehamishiwa Ofisi ya Rais, hazikaguliwi na Mkaguzi, na siyo tu hivyo, amesoma Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani hapa, anasema katika sehemu ambayo tunaonyesha hasara kubwa katika Taifa hili ni katika Mamlaka ya Ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo haja kubwa sana ya kuliangalia suala hili kwa sababu kuna kioja kimoja kiliwahi kutokea kwenye Bunge moja nilikuwa nasoma kwenye mitandao, wakati mwingine tunaweza tukawa tunapiga makofi kumbe tumetukanwa. Yule Mbunge alisimama akasema, nusu ya Wabunge walioko humu ndani ni wajinga! Watu wakasema afute kauli, afute kauli, akafuta kauli akasema, nusu ya Wabunge waliomo siyo wajinga! Wakapiga makofi! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine tunaweza kuwa tunalitukanisha Bunge letu bila sisi kujua kutokana na matendo yanayoendelea. Kinachoonekana, katika suala la kuhamisha mamlaka, anayenunua ndege ni Ofisi ya Rais, akinunua nzima, akinunua mbovu ni juu yake. Halafu huyo huyo ndiyo anapitisha bajeti ya matengenezo ya ndege, iwe labda alinunua nzima au mbovu! (Makofu)

Mheshimiwa Mwenyekiti, akitoka hapo huyo huyo ndiyo ananunua mafuta kwa ajili ya hizo ndege bila kujali fuel consumption ya ndege kama ilizingatiwa wakati wa manunuzi. Ipo haja ya Bunge kujitafakali kwa nini tumetoa mamlaka ya usimamizi wa ndege za Serikali, kutoka Wizara ya Ujenzi, tukapeleka Ofisi ya Rais, ipo haja ya kujitafakari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye matumizi ya wakandarasi, ipo dhana potofu ambayo Serikali ya Chama cha Mapinduzi inawaaminisha wananchi kwamba wakandarasi wazawa ndiyo ambao wanapewa kazi nyingi. Nataka nilieleze Taifa leo hii, ni kweli asilimia 85 ya wandarasi wa kitanzania ndiyo wanaopewa kazi, lakini ile asilimia 15 ya wakandarasi kutoka nje, ndiyo wanaolipwa zaidi ya asilimia 85 ya fedha zinazokwenda kwenye Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuone ile asilimia kubwa inayopewa, ndiyo inayokwenda nje ya nchi, hao wakandarasi wanaoitwa wazawa, wanapewa kazi za kawaida ambazo asilimia 15 tu ya bajeti ndiyo inatumika kuwalipa. (Makofi)

MHE. JOHN W. HECHE: Wanapewa kuchimba mitaro.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye Mamlaka ya Hali ya Hewa…

NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Katika Mamlaka ya Hali ya Hewa…

NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, anapotosha.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Si una muda wa kujibu baba!

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITIl: Taarifa, taarifa, taarifa! Mheshimiwa Heche, Mheshimiwa Heche kaa chini, Heche kaa chini.

MHE. JOHN W. HECHE: Is wrong!

MWENYEKITI: That is not wrong, kaa chini!

MHE. JOHN W. HECHE: Is wrong!

MWENYEKITI: You are wrong kaa chini!

MHE. JOHN W. HECHE: Siyo utaratibu!

MWENYEKITI: Sikiliza Mheshimiwa Heche, Bunge linaendeshwa na taratibu zake, huwezi ukaamuka tu na mkali yako ukasimama ukasema unavyotaka, kwanza sijakuruhusu usimame. No! No! anaweza kwa any time aka-inter, aka nini, tulia. Mheshimiwa Waziri!

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kitabu cha bajeti, Wizara inanunua ndege na utaona hapa katika ukurasa wa 467, kwa hiyo, nimelazimika kusimama kwa sababu dada yangu Mheshimiwa Makamba anatupotosha, analipotosha Bunge lako.

MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa Makamba!

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Waziri una nafasi ya kujibu, nafasi yako itakuja mwishoni, na mimi nafanya hivi kuisaidia Wizara yako, kwa sababu, Mheshimiwa Waziri, suala la ununuzi wa ndege zote zilizonunuliwa leo hii, hakuna performance inayoonekana katika Taifa hili zaidi ya hasara. Ukitetea kwamba wewe ndiye unayenunua utakuwa answerable at the end of the day na ninasikia vibaya sana kwa sababu wewe ni baba yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niongelee habari ya Mamlaka ya Hali ya Hewa, wiki iliyopita, Waziri alikuja hapa akasema kwamba kuna hali ya taharuki katika hali ya hewa, Lindi na Mtwara watapatwa na matatizo makubwa sana, tukasema sawa. Hii mamlaka ya hali ya hewa, ku-bate kuhusu mamalaka ya hali ya hewa ni afadhari u-bate game ya Yanga na Lipuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafuriko na madhara makubwa yamekwanda kutokea Shinyanga, Kahama, Mwanza, badala ya Lindi na Mtwara. Nataka kuhoji, hivi hawa watu wa mamlaka ya hali ya hewa ni wapiga lamri au ni professional people wamewekwa kwa ajili ya kutusaidia! (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nihoji tu kuhusu hao watu, na kwa nini hawawajibishwi? Wanaleta taharuki kwenye hii nchi na wanamwangusha Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Rais, mama anajitahidi kweli kuongea kwa ajili ya Chama cha Mapinduzi. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu suala la ucheleweshaji wa mizigo, I do no, shida ya mitandao. Tulitenga fedha nyingi sana hapa tena mkaja kwa mbwembwe kuhusu TTCL, leo hii Mheshimiwa Waziri haoni hata aibu kusema tumewapa VIATEL, anajibu maswali ya Wabunge hapa, ananadi makampuni ya nje, hivi hii TTCL imeshindwa kufanya kazi au kuna tatizo gani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mmeshindwa, si mtoe tu tamko kwamba, jamani na makampuni mengine yaje ili waendelee kufanya kazi. Mheshimiwa Waziri, siyo uzalendo, siyo uzalendo kuja kujisifia hapa kwamba umeimarisha au umesambaza mitandao ya makampuni ya nje, wakati TTCL tumekupa fedha hapa na umeshindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niongelee kwa haraka kuhusu Mamlaka ya Bandari. Tunafahamu kuna kazi kubwa sana inafanyika na niwapongeze wafanyakazi. Katika eneo lolote la kazi, maslahi ya wafanyakazi yanakuja kwanza! Kinachotokea mamlaka ya bandari, yule Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari anawafanyisha watu kazi pale mpaka saa sita, saa saba za usiku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wabunge hapa maslahi yetu huwa yanakuja kwanza, niseme, mtu anatoka kazini saa sita za usiku, kesho asubuhi saa 12 kamili anatakiwa aripiti ofisini, hatuwezi kufanya kazi kwa kukiuka sheria za kazi katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, just kwa sababu tunalazimisha mipango ambayo tuliipanga bila kufanya consultation iweze kufanikiwa. Niombe sana, Mawaziri, muangalie sekta zenu mnazofanya kazi, kufanya kazi sema punda afe mzigo ufike, Tanzania tunafanya kazi kwa kuangalia kwanza maslahi ya wafanyakazi na ndiyo maana juzi hapa, jambo la kwanza Kambi Rasmi ya Upinzani ilisisitiza ni kuhusu maslahi na mishahara ya wafanyakazi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme jambo la mwisho, kuhusiana na suala la mitandao, tena nilikuwa nimesahau jambo la muhimu sana. Kule kwetu Kahama, zipo kata ambazo ndiyo zinaongoza kwa uzalishaji, wale watu hawawezi kutoka kata moja kwenda nyingine kwa sababu hakuna barabara, hawawezi kutoka kata moja kwenda kata nyingine kwa sababu hakuna mawasiliano ya simu, hawawezi kutoka kata moja kwenda kata nyingine kwa sababu tumewatelekeza wamekuwa kama wanaishi watu walioko kwenye ujima. Nitazitaja kata chache tu ambazo wao wamenituma kwa dhati nifikishe suala hili kwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo Kata ya Wendere, tunayo Kata ya Ngogwa, Kata ya Ubagwe, Kata ya Nyandekwa na Kata ya Uleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ridhaa yako, ningemuomba Mheshimiwa Waziri, akija kuhitimisha hapa leo, awaahidi wananchi hawa, ambao Mheshimiwa Rais anajinadi kwamba wasukuma ndiyo wamempigia kura. Hivi leo ni mwaka 2019, ni lini mtawatengenezea barabara, ni lini mtawapelekea mawasiliano ya simu, maana wale watu wanashida zote katika nchi hii, na mimi, yaani, ningekuwa siyo mpenzi wa watanzania ningesema afadhali msipeleke ili tuendelee kuchaguliwa chama cha CHADEMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme, kwa sababu nawapenda watanzania wenzangu, naomba nisisitize, Mheshimiwa Waziri, wapelekee wale watu huduma! Waonee huruma wanaishi maisha ya kijima.

MWENYEKITI: Ahsante, muda wako umekwisha.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utendaji uliotukuka kwa kipindi cha miaka minne ya Uongozi wake
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi na mimi nichangie Azimio hili la kumpongeza Mheshimiwa Rais. Kwa vile tumeamua kwenda na utamaduni huu wa kumpongeza Mheshimiwa Rais, basi niombe hasa Baraza la Mawaziri wamshauri mambo ambayo yeye mwenyewe moja kwa moja yuko responsible kuyatekeleza, wamshauri hilo ili isije ikatia doa hizo sifa nyingi ambazo wanampatia.

Mheshimiwa Spika, naomba tu nilifahamishe Bunge lako Tukufu kwamba Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndiyo Waziri mwenye dhamana ya TAMISEMI na mpaka leo tunavyozungumza pamoja na joto kali la matatizo makubwa yanayojitokeza katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mpaka leo Waziri wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli hatujasikia kauli yake juu ya Uchaguzi wa Serikali za uchaguzi wa Mitaa. Kwa hiyo mumshauri kwa sababu mwisho wa siku Wizara zenu ninyi Mawaziri zinakwenda vizuri lakini yeye Wizara yake imesua sua na kuna doa kubwa la Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nikukumbushe tu...

SPIKA: Mheshimiwa Salome kuna taarifa Chief Whip amesimama hapa.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika,
naomba kumpa taarifa mchangiaji wa Azimio hili zuri sana la kumpongeza Rais wetu Dkt. John Magufuli kwamba Ibara ya 34 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inampa madaraka Mheshimiwa Rais kukasimu majukumu yake kwa Baraza lake la Mawaziri na watendaji wengine ambao watamsaidia kutekeleza majukumu mbalimbali ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu hilo limefanywa vizuri sana na Waziri aliyekasimiwa madaraka hayo, Waziri wa TAMISEMI, ndugu yetu Mheshimiwa Selemani Jafo na hivi tunavyoongea Watanzania wote ni mashahidi, Mheshimiwa Selemani Jafo ameshafanya kazi yake ya kueleza kila kilichojiri katika uchaguzi huu, taratibu zilizotakiwa kufuatwa na maamuzi ya Serikali katika jambo hilo. Kwa hiyo kuendelea hapa kumng’ang’ania Mheshimiwa Rais, kwanza pia ni kuvunja kanuni ya kiutaratibu, kanuni 64(1)(c) kinachotupa mwongozo wa kuzungumza masuala na mwenendo wa Rais katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba unapokea taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo siipokei amesema mwenyewe kwamba amekasimu madaraka kwa Mheshimiwa Jafo na sisi Vyama vya Upinzani Tanzania nzima hatujaridhishwa na maamuzi yaliyotolewa na Serikali kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa, kwa hiyo tunahitaji Waziri mwenye dhamana atoke atoe kauli juu ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo ningependa Baraza la Mawaziri wamkumbushe Mheshimiwa Rais, hivi tunavyoongea tangu 2015 tumekuwa tukijadili bajeti humu ndani na kupitisha, Wizara karibu zote hazijapelekewa angalau asilimia hamsini ya bajeti yake, hiyo inamaanisha kuna mdodoro mkubwa wa uchumi…

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …na maendeleo kwenye nchi yetu. Mumkumbushe Mheshimiwa Mheshimiwa Rais kwamba tunahitaji…

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …sisi Wabunge ni wawakilishi wa wananchi tunayoyaleta ni mapendekezo ya wananchi…

SPIKA: Mheshimiwa Salome…

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …pesa zipelekwe kwenye hayo maeneo ili wananchi waweze kupata maendeleo.

SPIKA: Mheshimiwa Salome kuna taarifa uipokee.

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Getere nimekuona.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Salome anayeongea unajua kuna vitu vingine unaongea kwa kukariri makaratasi. Hivi kama kweli hela haziendi majimboni, haziendi kwenye halmashauri kwenye mikoa, hivi haya mambo yote ambayo yanayotajwa barabara za lami, hospitali, shule, na vitu vingine, vitu vyote vinavyotajwa hapa vinafanya biashara gani? Hivi labda kuna hela zinatoka mbinguni zinaenda kufanya kazi ya maendeleo kwenye maeneo hayo au zinatoka wapi?

SPIKA: Taarifa inakwambia Mheshimiwa Salome tangu uwe Mbunge kuna mshahara unaodai, mbona Magufuli amelipa mishahara yako yote. (Makofi/Vigelegele)

Ndiyo taarifa anayoitoa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba Baraza la Mawaziri na Wabunge wa CCM wamkumbushe Mheshimiwa Rais, kuna mambo yanaendelea ndani ya nchi hii ambayo ni very serious, kuna watu wanauawa kwenye nchi hii, kuna watu wamepotea kwenye nchi hii, mpaka leo Mheshimiwa Tundu Lissu alipigwa risasi, hatujasikia kauli yake juu ya matatizo yanayoendelea kwenye nchi hii, mnapompongeza inamtia doa Mheshimiwa Rais Mwenyewe, wamkumbushe tunahitaji kusikia kama Rais…

SPIKA: Mheshimiwa Salome umetumia neno…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, naomba tusikilizane. Mheshimiwa Salome umetumia neno kuna watu wanauawa, kidogo ni neno hatari katika nchi hii, Watanzania wakisikia maneno kama hayo basi ni vizuri uka-qualify kidogo.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, kwa heshima na taadhima kuna Diwani wetu anaitwa Lenwa anaishi kule Morogoro, iliripotiwa kwenye vyombo vya habari kwamba ameuawa na watu wasiojulikana. Kwa heshima na taadhima, Mheshimiwa Mawazo aliuawa na kesi yake mpaka leo ipo mahakamani, hatujapata hatima ya kesi yake na watu hao…

SPIKA: Mheshimiwa Salome unajua kabisa jambo ambalo lipo mahakamani haliruhusiwi kujadiliwa hapa.

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Ndiyo nasema Mheshimiwa…

SPIKA: Tuongee mengine siyo ya Mahakamani.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, sawa. Naomba niendelee; katika nchi hii kuliwahi kutokea saga la makinikia na Mheshimiwa Rais alikuwa mbele sana kusimamia saga hii na sheria zililetwa tukapitisha hapa Bungeni kwamba hakuna jambo lolote litafanyika mpaka Bunge hili lipate habari. Tumesubiri kwa muda mrefu wananchi wangu wa Shinyanga wanasubiri Noah, tulichokipata leo ni kauli ya Mheshimiwa…

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …amekuja na kampuni yake ya Twiga, tunataka kujua mustakabadhi ya kesi ya makinikia…

SPIKA: Mheshimiwa Mlinga, Mheshimiwa Salome, kuna taarifa. Mheshimiwa Mlinga.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …imefikia wapi ili tumpongeze Mheshimiwa Rais.

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

SPIKA: Naomba tusikilizane, Mheshimiwa taarifa yako iwe kwa kifupi.

T A A R I F A

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nataka nimpe taarifa mzungumzaji anayezungumza, suala la makinikia siyo dogo kama anavyolifikiria yeye. Katika chama chao michango tu ya Wabunge zaidi ya milioni 300 mpaka leo vikao vinakalika usiku na mchana bado haijapata jawabu, michango ya Wabunge imeenda wapi? Kwa hiyo suala la makinikia siyo dogo kama anavyolifikiria yeye, waanze kwanza na michango ya Wabunge.

SPIKA: Mheshimiwa Salome, bado muda uko kwako, malizia tu maana naona kuna nusu sekunde tu hapo.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie Mheshimiwa Mlinga kwa taarifa yake siipokei na mwisho kabisa.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …wakati mnaendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais, naomba mumkumbushe nchi hii ni nchi ya vyama vingi na kila chama kina haki ya kufanya siasa ili kiweze kujiendeleza na kukua.

SPIKA: Ahsante sana, kengele imeshalia.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa muhimu sana.

SPIKA: Tunahitaji kufanya mikutano ya hadhara ili tushindane kwa hoja na siyo kushindana kwa…

SPIKA: Kengele imeshalia Mheshimiwa Salome.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, Mwenyezi Mungu akubariki. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti kuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaanza, nimsaidie kaka yangu Marwa Ryoba, kaka yangu wa zamani kwamba ukitembea na Ilani ya Uchaguzi ya CHADEMA ujitahidi upate na vitabu vingine vitatu vitakusaidia sana. Najua una kazi kubwa sana uko ulipo, tafuta Sera ya CHADEMA ambatanisha na Mpango wa Utekelezaji wa Bajeti na bajeti kivuli ya CHADEMA. Hapo utakuwa umefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muugano wa Tanzania ….

TAARIFA

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome, kuna taarifa, Mheshimiwa Ryoba.

MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa, kwa wale tuliogombea kupitia CHADEMA…

MBUNGE FULANI: Yeye hajagombea.

MHE. MARWA R. CHACHA: Document tuliyopewa ni Ilani, CHADEMA haikuwa na Sera, juzi tu ndiyo wametengeneza Sera, hawajawahi kuwa na Sera, wana hii Ilani.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

MBUNGE FULANI: Yeye hajagombea.

MHE. MARWA R. CHACHA: Huyo ni Viti Maalum hajawahi kugombea Ubunge.

(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Wycliffe Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 8(b) inasema: “Serikali ili kuhakikisha kwamba inatekeleza majukumu yake ni lazima ihakikishe inaweka ustawi wa watu”. Nasema hivi, Mbunge yeyote aliyemo humu ndani ambaye ataunga mkono bajeti hii ya Mheshimiwa Dkt. Mpango halafu akajiita mzalendo nitamshangaa. Nasema hivyo kwa sababu zifuatazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii ya Mheshimiwa Dkt. Mpango imekwenda kupeleka asilimia 39% ya bajeti yote kujenga Stigler’s na SGR, maendeleo ya vitu. Bajeti hii inakwenda kinyume na dunia inayokwenda, dunia kwenye Sustainable Development Goals Stigler’s kwa maana ya miundombinu na nishati ni kipaumbele Na.7 na Na.9. Kipaumbele Na.1 ni kufuta umasikini; Na.2 ni kuhakikisha hakuna njaa kwenye nchi; Na.3 ni afya; Na.4 ni elimu bora; Na.5 ni usawa wa kijinsia; Na.6 ni maji safi na salama, sasa ndiyo unakuja Na.7 nishati nafuu kwa maana ya Stigler’s Gorge then unakuja Na.8 kazi yenye staha na Na.9 ni miundombinu ambayo ndiyo SGR. (Makofi)

TAARIFA

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, kuna taarifa, Mheshimiwa Kuchauka.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumpa taarifa mzungumzaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati jana nachangia nilisema kwamba asilimia 65% ya watu wetu wanategemea sana kilimo na nikaainisha moja ya matatizo ya kilimo ni miundombinu ambayo ingewezesha wakulima wetu kufikisha mazao yao kwenye masoko. Nikazungumzia suala la reli na barabara. Sasa anaposema kwamba Serikali hii inaingiza fedha nyingi kwenye miundombinu inaacha maendeleo ya watu hapo namshangaa. Maendeleo ya watu yanakuja baada ya kuimarisha miundombinu ili wakulima waweze kutoa mazao yao mashambani na kuyafikisha kwenye masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa hiyo. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, unilindie muda wangu, tafadhali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa lugha nyingine msemaji aliyetoka kunipa taarifa anamaanisha kwamba Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi, Serikali ya wanyonge imepeleka ile shilingi trilioni 33.1 ambayo leo tunatamba ndiyo bajeti ya Serikali, hayo anayoyasema yeye ni shilingi trilioni nane tu, pesa nyingine yote wamekwenda kuboresha miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni kwamba kununua dawa tunapambana kwenye trilioni nane, Wabunge 395 tuliopo humu ndani dawa ni trilioni nane hiyo tunagombania, kupunguza udumavu wa wananchi trilioni nane, kwenda kumtua mama ndoo kichwani kelele zote trilioni 8 na kuinua kilimo trilioni nane; kwa mwaka huu wote wa fedha na mambo mengine yote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pesa nyingine yote ambayo iliyopo inakwenda kulipa deni la Taifa trilioni tisa, kwenye mishahara trilioni saba trilioni tatu matumizi mengineyo na kwenye pesa ya maendeleo hiyo trilioni nane usisahau ndiyo tunapoenda kutoa hela ya Stiegler’s na SGR yaani reli ya kati na huo mtambo wa kufua umeme wa Mto Rufiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii Serikali inaturudisha nyuma ambako hatukuwahi kufikiria. Hivi jiulize swali, mwaka jana wamesema projection zao ilikuwa ni kukusanya trilioni 1.4, wakakusanya trilioni 1.2. Na hiyo pesa wameikusanya alisema hapa Mheshimiwa Lwakatare, walitumia mizinga ya aina zote; matrafiki wakapanda juu ya mti, DPP akapeleka kesi, huku wajasiliamali vitambulisho 20,000, kila aina ya mbinu wakaishia 1.2 trilioni. Sasa angalia sasa hivi wana- projection ya kukusanya 1.6 trilioni, tutapona kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vipaumbele vyao sasa vya kufikisha 1.6, wanaenda kuweka kodi kwenye peremende, wanahangaika na mawigi, wanakwenda chocolate waweke kodi, leo wametoa VAT kwenye taulo za kike. Hiyo ndiyo aina ya wataalam tulionao kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, atakayeunga mkono bajeti hii nitamshangaa. Kwanza imewekeza kwenye vitu lakini pili pesa yote ya kuendesha miradi inatokana na wananchi wenyewe…

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: wanasema asilimia 15 ya bajeti watatoa kutoka kwenye…

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa ya mwisho hiyo kwa Mheshimiwa Salome Makamba

T A A R I F A

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nataka nimueleweshe ndugu yangu Mheshimiwa Salome Makamba kwa sababu yeye ni mwanasheria, mimi ni administrator by professional. Unapotaka kujua pesa kiasi gani imepelekwa kwenye Sekta ya Elimu usiangalie Wizara ya Elimu pekee, nenda kaangalie TAMISEMI, Utumishi na Elimu yenyewe. Na hata Wizara ya Afya ukitaka ujue pesa kiasi gani imepelekwa kwenye Sekta ya Afya nenda kaangalie TAMISEMI ndiyo utakuta ujenzi wa miundombinu, vituo vya afya na Hospitali za Wilaya na Wizara ya Afya yenyewe pamoja na Utumishi mishahara ya madaktari. Kwa hiyo, usiangalie Wizara ya Afya, nenda kaangalie na Wizara nyingine. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, hapana, naomba niendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasema kwamba asilimia 85 ya makusanyo ya Serikali wanakusanya mapato kutoka kwa wananchi mapato ya kikodi yaani hizo njia walizokuwa nazo na peremende na kila kitu wanatafuta asilimia 85 ambayo mwaka uliopita walifeli. Asilimia 15 wanategemea wafadhili na mikopo nafuu kutoka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa angalia picha inavyokwenda, hawa wafadhili mwaka jana kwa mujibu wa Ripoti ya UNESCO walikata misaada Tanzania kwa zaidi ya asilimia 49. Na haya yote wameyasema kwa nini wamekata mikopo hiyo, wamekata mikopo na wamekata misaada. Hali ya demokrasia nchini siyo shwari, utawala bora hakuna, uhuru wa vyama vya siasa hakuna, hivi hao watu mnaotegemea watawapa hiyo asilimia 15 itatoka wapi? Wanakwenda kuwakamua Watanzania kwa kiwango ambacho mzalendo yeyote aliyepo humu ndani hawezi kukubaliana na hii bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siwezi kukubali Mheshimiwa Dkt. Mpango ku-support bajeti yako mpaka utakaponieleza ni vyanzo vipi vya uhakika ulivyojiandaa navyo vya kupata pesa kwa ajili ya kuendesha bajeti yako. Mpaka utakaponieleza ni lini utaboresha private sector ambayo ndiyo engine ya uchumi wa nchi, utaiboresha lini ili uitoe Serikali kwenye matrilioni ya kununua ndege, kujenga SGR na kwenda kujenga sijui mradi wa Mto Rufiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya mambo yafanywe na private sector, ninyi mtekeleze Katiba ya nchi yetu kama livyoapa kuilinda kwa kwenda kufanya maendeleo ya watu badala ya kufanya maendeleo ya vitu. Sitopiga kura ya ndiyo kwenye bajeti hii ya Serikali ya mwaka 2019/2020. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hotuba hizi mbili za Katiba na Sheria na Kamati yangu ya Sheria ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo napenda kuongea mambo machache. Kwanza, napenda kuongelea misingi miwili ya Utawala Bora katika nchi yoyote inayoendeshwa Kidemokrasia. Misingi miwili nitakayoiongelea, wa kwanza ni mgawanyo wa madaraka, kwa maana ya separation of power na wa pili ni uwajibikaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yoyote inayotambua misingi hii miwili ya Utawala Bora, ni lazima, siyo tu itekeleza misingi hii, lakini pia ionekane kwamba inatekeleza kwa vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi, hasa kwenye upande wa mgawanyo wa madaraka, Tanzania katika uendeshaji wa shughuli za Serikali, tunayomihili mitatu, kwa maana ya Mahakama, Serikali na Bunge. Juzi tulikuwa na Siku Maalum ya Sheria hapa Tanzania. Katika siku hiyo Maalum, iliyofanyika karibu nchi nzima, kitu kinachotarajiwa kwenye siku ile, viongozi wa Judiciary wanategemewa kuitumia siku hiyo kama siku maalum kujadili changamoto na namna bora ya uendeshaji wa Mahakama katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kikubwa ambacho nilikishuhudia kinaendelea, ni namna ambavyo Judiciary wanawapa nafasi watu wa Executive (Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa) kwenda kutangaza yale ambayo wanayafanya kwenye Serikali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko forum mbalimbali ambazo tunaweza kuzitumia kutangaza haya tunayotangaza, lakini siku ya Wanasheria Duniani Watanzania wangependa kusikia ni namna gani Judiciary wamejielekeza kupunguza mlundikano wa kesi zisizokwisha Mahakamani, ni namna gani wanapunguza mahabusu waliolundikana Magerezani, ni namna gani wanaongeza Mahakama, ni namna gani wanaongeza Mahakimu na Majaji, katika nchi hii, ili siyo tu haki itendeke, bali ionekane imetendeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawaona Majaji na ilitokea Iringa kule, picha moja inazunguka kwenye mitandao. Jaji na Mkuu wa Mkoa, Jaji ki-hierarchy ni mtu mkubwa sana. Sijui kama wamejawa na hofu, sielewi. Jaji anatembea pembeni, kwenye Red Carpet anatembea Mkuu wa Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali itekeleze mambo yake ya Executive na iiache mhimili wa Mahakama uweze kufanya kazi kwa uhuru, ufanye kazi kwa weledi na utashi. Kwa sababu pamoja na kuhubiri maeneo mbalimbali kwamba haki inatendeka, haipaswi...

T A A R I F A

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nataka niishauri Serikali, iliwekwa misingi ya Utawala Bora, iliwekwa misingi ya Uwajibikaji, yote hiyo ni kutoa sintofahamu na kutoa ombwe kubwa ambalo lilikuwepo la kuonekana mihimili hii inaingiliana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, kwa wale wanaosoma, Wanazuoni, huu mjadala ni mkubwa sana. Nawaomba sana, Serikali, Mahakama na Bunge, kuepusha maneno yanayojitokeza ya kuonyesha kwamba mihimili hii inatawaliwa na mhimili wa Executive. Hebu tuoneshe kwa vitendo kwamba tunaweza kujisimamia, kwamba tunaweza kutekeleza wajibu wetu kwa mujibu wa Katiba na Sheria na Katiba inatulinda kufanya hivyo.

T A A R I F A

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye hoja ya pili kuhusu Tume Huru ya Uchaguzi, ni lazima kila mtu awajibike kwenye eneo lake. Leo Mheshimiwa Selasini ameeleza vizuri kuhusu uchaguzi wa Serikali za Mitaa; na Mheshimiwa Waziri wakati anajaribu kujibu, anasema jambo hili linafanyika kwa uwazi. Sisi ni Wabunge, ni Wawakilishi wa Wananchi, tunasimama hapa kutoa maoni na mapendekezo yetu ya namna bora ya kushiriki katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Nafikiri Mawaziri wangetumia fursa hii kusikiliza maoni yetu, kuyasimamia, kuyatekeleza kwa mustakabali wa Taifa hili kuliko kusimama kuwa defensive, kwa sababu haimsaidia mtu yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaelekea kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Chaguzi kwenye nchi hii ni moja kati ya kitu ambacho kinaweza kutuletea matatizo ambayo yanaweza kuvunja amani. Tusipoandaa uchaguzi huu kwa kufuata taratibu za ushirikishwaji wa wadau…

T A A R I F A

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoelekea katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, sisi Wabunge, moja kati ya jukumu letu ni kuhakikisha kwamba tunaisaidia nchi hii kuwapa uelewa mzuri wa yale tunayoyatunga humu ndani wananchi wetu, kuwasaidia kuwafikishia taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunakuja kukutana hapa Bungeni tena mwezi wa Nne, tukitoka hapa ni mwezi wa Saba. Tunamwomba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI aweke uwazi wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa ili tunapotoka hapa, moja kati ya majukumu yetu iwe ni kwenda kuwaelimisha wananchi na kuwapa taarifa juu ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, anasema hiyo kazi inafanywa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki ndicho kinachofanya leo na kesho sisi Wabunge tutukanwe na kuonekana hatuna maana. Tunatoa ushauri, Serikali inaelewa kuliko sisi tunaowakilisha wananchi. Mwisho wa siku, ndiyo kauli zinapozuka mtaani, unazisikia zile; kama ile aliyosema CAG, sijui ameshaomba radhi!

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais alipohutubia Bunge hili kwa mara ya kwanza. Moja kati ya kitu Mheshimiwa Rais alisema, ni lazima tufute tozo za kero kwa wananchi kwa sababu zinapunguza ufanisi na zinazuia wananchi kufanya shughuli za maendeleo. Juzi Mheshimiwa Rais ameanzisha kitu kinaitwa Vitambulisho kwa Wajasiriamali.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie kwenye mapendekezo haya ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na wa Mwaka Mmoja. Wamezungumza wengi lakini mimi napenda nianze kwa kutafuta tumekwama wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nasoma Mpango huu wa Tatu wa Serikali ilibidi nirudi nyuma niangalie Mpango wa Pili na Mpango wa Kwanza wa Maendeleo. Ukiangalia Mpango wa Pili wa Maendeleo ambao ndiyo tunaumaliza, Serikali kwenye eneo la ukuaji wa uchumi, ilikuwa imepanga kukuza ukuaji wa uchumi mpaka asilimia 10 ifikapo mwaka 2021. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyoanza tu ule Mpango mwaka 2016 tulianza na 7%. Tulipoanza tu Awamu hii ya Tano 2016 tukaporomoka kutoka 7% mpaka asilimia 6.8. Tukajipanga vizuri, mwaka uliofuata mwaka 2017/2018 tukarudi asilimia 7%. Hivi ninavyozungumza, tangu Awamu ya Tatu ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi, kiwango cha ukuaji wa uchumi kimebaki 7%. Tafsiri yake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni kwamba ukuaji wa uchumi katika nchi yetu ya Tanzania umesimama tangu mwaka 2001. Kwa maana hiyo, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwenye Mpango wa Kwanza, Mpango wa Pili tumeshindwa kufikia angalau target ambayo tumejiwekea wenyewe ya asilimia 10 ya ukuaji wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, target hii iko kwenye Mpango, yaani Serikali wamejipangia wenyewe. Ni sawa na mtu unaenda kuposa ukaambiwa jipangie mahari; ukasema nitatoa Sh.50,000/=. Haya basi lipa, halafu unasema sina. Hapo sasa ndipo tunapoanza kukwama kwenye Mpango wa kuwasaidia wananchi kuwatoa kwenye umasikini. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende kwenye pato la kila mmoja. Kwenye Mpango wa Pili ambao ndiyo tunaumaliza, Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi ilisema itahakikisha Mtanzania anaongeza pato lake mpaka Dola 1,500 kwa mwaka ifikapo mwaka 2021. Wakati huo inaingia Awamu ya Tano, kipato cha mmoja mmoja kwa Mtanzania ilikuwa ni kama dola 1,043 na kasi zote, makofi yote na ngonjera zote tunazozipiga, tumejivuta wee, kutoka Dola 1,043, tumefika Dola 1,080; tumeongeza Dola 37 kwa mwaka. Yaani shilingi tuseme kama 6,000/= hivi kwa mwezi kwa kila Mtanzania yaani hizi kelele zote tunazozisikia. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kwa miaka mitano tumeweza kuongeza Dola 37 tu kwenye pato la Mtanzania mmoja mmoja, tafsiri yake, ili tufike kwenye target ya Dola 1,500 kwa kila Mtanzania, tunahitaji miaka 60. Hiyo ndiyo tafsiri. Kwa sababu miaka mitano tumeongeza Dola 37, tukiongeza miaka mitano mingine tutafika Dola 74 au tutashuka, hatuwezi kujua. Kwa sababu ikiisha hii kumi, hatujui atakayekuja atakuwa na kasi gani? (Kicheko)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome kuna Taarifa upokee. Nilishawaambia hali ya hewa itachafuka hapa. Naona dalili za mawingu. (Kicheko)

Ni Mheshimiwa nani? Ni Mheshimiwa Kingu, karibu.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe dada yangu Salome Taarifa kwamba, ukuaji wa uchumi na suala zima la per capita income lazima lijengewe base ambazo zikisha-mature zitakwenda kuleta spill over impact kwa individual citizen. Uwekezaji unaofanywa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi katika kuwekeza katika Sekta ambazo zitafanya transformation kwa mfano Sekta ya Umeme, Miundombinu pamoja na Miundombinu ya Kilimo hicho wanachokisema cha mwaka mmoja kukua kwa hizo dola anazozitaja ni upotoshaji. Nataka nimhakikishie Tanzania na uchumi wake utakwenda kubadilika kulingana na mipango Madhubuti ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

MWENYEKITI: Salome unaelimishwa kwamba hiyo hesabu yako inaweza ikawa hivyo kwa ile lugha ya wenzetu if everything remains constant. Sasa nani kakwambia tunakokwenda ni constant? Kwa uwekezaji anaousema kutakuwa na faster growth. Unapokea Taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Kingu atulie. Tujadili haya mambo, Mheshimiwa Rais ana mategemeo makubwa sana na Bunge hili, tujadili haya mambo tumekwama wapi halafu nitashauri tunatokaje tulipo. Ndiyo maana nikasema kama tumeongeza dola 37 kwa pato la mtu mmoja kwa miaka mitano. Itatuchukua miaka 60 ili tufikie malengo ya pato la mtu mmoja liweze kufika dola 1500. Hapo sasa, if all factors remain constant, hapo ndiyo tutafika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hili jambo hili linasemwa uchumi wa kati, watu wanasema hela hatuna mfukoni na ni very confusing na nashauri tu Wabunge tupewe semina ya uchumi wa kati unavyotakiwa ku-reflect pesa zilizoko mifukoni mwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya kiwango cha umaskini nchini, Serikali hii ya Chama Cha Mapinduzi hasa Serikali ya Awamu ya Tano wakati inaingia madarakani iliahidi kupunguza kiwango cha umaskini kwa asilimia 11.5, kwamba watatutoa kwenye kiwango cha umaskini kutoka asilimia 28.2 mpaka asilimia 16.7. Sasa mpaka tunamaliza mpango huu wametutoa asilimia 28 mpaka asilimia 26 na pointi, sawa na asilimia 1.8. Sasa nina lengo kubwa sana la kuisaidia hii Serikali na mimi bado ni kijana. Kwa mwendo huu tunaokwenda nao kuna mawili; ama hatuwapi nafasi wachumi wetu kutushauri vizuri tuweze kuwa na mpango unaoendana na uhalisia au tunamwogopa Mheshimiwa Rais kumweleza ukweli, tunaamua kumpamba kwa maneno mazuri lakini kiukweli hali ya kiuchumi ni mbaya. Kuna hayo mawili. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kusema tumekuja kwenye uchumi wa kati, wananchi hawalielewi kwa sababu hali ya umaskini katika nchi hii ni kubwa. Ni zaidi ya asilimia 26.2, kwa hiyo ukisema tumeenda kwenye uchumi wa kati wakati watu bado ni maskini lazima watu wachanganyikiwe. Matokeo yake, tunavyo-promote kwamba tuko kwenye uchumi wa kati, tunajitoa kwenye level ya nchi inayostahili misaada…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome ngoja upewe Taarifa kidogo. Jitambulishe.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naitwa Kingu.

MWENYEKITI: Aaa, bado Mheshimiwa Kingu unaongea tena.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa Taarifa dada yangu Salome.

(Hapa baadhi ya Wabunge walzungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Naomba mtulie this is democracy. Naomba kumpa dada yangu Salome Taarifa kwamba nchi kuingia kwenye uchumi wa kati kuna stage. Naomba dada yangu Salome atulie asome principles za ukuaji wa uchumi na masuala mazima ya global economy. Stage za nchi kuingia katika uchumi wa kati haimaanishi kwamba tumeshafika katika bar ya juu ya per capita income of individual na hicho ndicho Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inajenga misingi sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeingia katika uchumi wa kati, tuko katika class ya chini, ndiyo sasa hivi tunajenga mipango hapa kutaka kuijenga nchi na kupeleka kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome pokea.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo Taarifa siipokei na kwa sababu ya muda, naomba niendelee na Mheshimiwa Kingu naomba utulie kidogo, acha hayo mambo. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali tuliyonayo ya kiuchumi mifukoni watu hawana kitu ndiyo inayosababisha watu wasielewe maana ya nchi kuingia katika uchumi wa kati na kwa maana hiyo hata Serikali yenyewe imechanganyikiwa kwenye hilo. Tumeingia kwenye uchumi wa kati tunajisifu. Nchi ikishaingia kwenye uchumi wa kati inaingia kwenye class ya nchi ambazo kuna baadhi ya mambo lazima tukose, tutakosa misaada mbalimbali, misamaha mbalimbali ya kikodi, scholarship za wanafunzi. Tunajikuta kwa sababu ya kukosa, kwa sababu tuko kwenye uchumi wa kati…

MWENYEKITI: Nimekuona Mheshimiwa Kimei. Mheshimiwa Salome subiri Mheshimiwa Kimei…

T A A R I F A

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii. Naomba niseme hivi, fedha iliyo mfukoni haihesabu kama wewe ni tajiri au sio tajiri. Kitu kinachohesabika ni kuna fedha unayopata wewe kama kipato chako, mshahara au umeuza mazao yao inaingia mfukoni kwako unalipa na kodi na kadhalika. Kinachojalisha sana ni zile huduma unazopata kutoka Serikali za bure. Huduma za bure kama elimu, watoto wanasoma bure. Hiyo shilingi ambayo ulikuwa ulipie mtoto wako anaenda shule si umeweka mfukoni? Unaibakiza mfukoni kwako. Ukipata matibabu ambayo yana ruzuku si hela inabaki mfukoni ya ziada? Ukipanda gari ambalo ulikuwa ulipe shilingi 1,000 ukalipa shilingi 500 kwa sababu barabara ni nzuri si hela inarudi mfukoni, si utajiri unaongezeka? Utajiri hautokani na ile hela ambayo lazima uwe nayo. Tuangalie pia kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imetupa huduma gani za ziada ambazo hazilipiwi na ambazo zinarudisha fedha zetu mfukoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe angalizo moja. Fedha ambayo tunapewa inaenda moja kwa moja kwenye huduma hizi inasaidia zaidi kwa sababu kuna wengine walikuwa wanapata hela wanakunywa tu. Hata hawapeleki watoto shule, wanaacha shule. Sasa watoto wale wanaenda kwa hiyo inakuwa kwa welfare of the society ni kwamba hiyo inakuwa ina-contribute sana. Tusiangalie tu hela ya mfukoni, hela ya mfukoni haina maana! Hela ya mfukoni is not so much important. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kimei. Actually, ndiyo maana alisema kwamba Wabunge tunahitaji semina. (Makofi)

Mheshimiwa Salome malizia.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niongeze tu kwenye hilo neno lako ulilolisema, kwanza Taarifa siipokei na awe makini sana kwa sababu ni Mbunge wa Jimbo, unaposema tusiangalie tu hela ya mfukoni tunaongelea habari ya hali ya wananchi kuweza kufanya manunuzi ya bidhaa. Per capita income watu hawana hela. Serikali inajinasibu iko kwenye uchumi wa kati kuna watu wako Muamalili kule Chibe hawawezi ku-afford kununua kilo moja ya unga, yeye alikuwa Mkurugenzi wa CRDB, tunaongelea wananchi maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Sasa naomba nimlinde ili amalizie na sababu yake ni kwamba ni katika walio wachache na wao kutwa nzima ya leo wanachangia wawili tu. Kwa hiyo tuvumilie kidogo tusikilize mawazo ya upande wa pili. (Makofi)

Kwa hiyo, Salome nakupa dakika tano ili umalizie sasa. (Makofi)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba nishauri yafuatayo: Wameleta mapendekezo ya Mpango. Warudi nyuma kuanzia mapendekezo ya Mpango wa Kwanza na wa Pili kwa sababu tumekwambia hapo. Warudi nyuma wakaangalie tulikosea wapi, kwa nini tuli-project kufika asilimia 10 na tumekwama kwenye saba tangu 2001 katika hali ya uchumi. Warudi hapo. Hiyo ni mosi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni lazima turudi kwenye mfumo shirikishi wa kiuchumi. Hatuwezi kuishi kwenye Serikali ya matamko, hatuwezi kuishi kwenye Serikali ya miongozo. Ni lazima wananchi, Sekta Binafsi na Serikali tushirikiane kwenye kukuza uchumi na nitatoa mifano miwili. Mfano kwa kwanza ni kuhusiana na hivi vitambulisho vya wajasiriamali. Yalitoka matamko hapa, presidential proclamation kwamba vitambulisho view shilingi 20,000 vikakusanywe. Jambo hilo halikueleweka. Tukienda kwenye hansard Wabunge waliomba ufafanuzi lakini kwa vile ilikuwa your wish is my command, lilikwenda, limekwama! Sasa wamelirudisha mwongozo kwenye Wizara. Mwongozo kwenye Wizara unasema Halmashauri zikatekeleze, wakatekeleze kwa mfumo upi? Ule ule wa Mgambo kupiga mama zetu ili wachangie 20,000? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unayo power ya kuagiza sheria hii iletwe Bungeni ishirikishe wadau, ifanyiwe scrutinization ili iweze kuendana na mfumo halisi wa maisha ya Watanzania. Mfumo huo huo uko kwenye kodi za mabango na majengo. Walitoa kwenye Halmashauri, Halmashauri zika-paralyse. Sasa hivi wamewarudishia lakini kimsingi hawajarudisha, ni vile hawana manpower ya kukusanya zile pesa wamepeleka local government zikusanywe, zinaingia kwenye mfumo wa control number zinaenda Hazina kurudi kwenye Halmashauri ni mtihani. Kwa hiyo lazima tuwasikilize wananchi, lazima Serikali isikilizwe na wananchi ni Bunge. Kabla hawajaenda kwenye hatua hiyo sisi wawakilishi wa wananchi ni lazima tushiriki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, mapendekezo yangu. Iko haja ya kutengeneza Kamati Maalum ya Bunge itakayofuatilia ahadi za Serikali na Viongozi Wakuu wa Nchi hii. Leo Waziri kanijibu hapa, bahati nzuri ulikuwa kwenye Kiti namuuliza ni lazima tupunguze ajali za barabarani, ni lini utaleta marekebisho ya sheria ananiambia sheria iko njiani amefunga makaratasi ameondoka! Sijui njiani ni Kibaigwa, sijui ni Manyoni, hakuna commitment! Watu tuko serious, we are using brain, watu wanafanya siasa ndani ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili Bunge lako ni Bunge makini, Mawaziri wageni mjue tunahitaji, na Kanuni zinasema lazima swali la Mbunge lijibiwe kikamilifu. Tutengeneze Kamati Maalum ya kufuatilia ahadi za Serikali na Viongozi Wakuu. Sasa hivi kila Waziri hapa anasema tutaongozana kwenda Jimboni kwako wanaenda kufanya nini, hatujui. Wakienda wanafanikisha hatujui. Tunataka tufahamu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho na sio kwa umuhimu, Mheshimiwa Mpango mwenyewe amesema kwamba ili tufanikiwe Mpango huu lazima tuwe na utawala bora lazima tuwe na amani, lazima tuwe na utulivu...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome na Mawaziri wanatakiwa wafuatane nao ni Mawaziri wanawake tu. (Makofi/Kicheko)

Malizia hoja yako dakika tano zinaisha.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema lazima tuwe na utawala bora, tuwe na amani, tuwe na utulivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo hayako sawa! Ni kwamba yametulia tumetoka kwenye uchaguzi. Yaliyotokea kwenye uchaguzi mnayajua, hatuwezi kuka kimya. Tutengeneze Tume ya Umoja ya Maridhiano ya Kitaifa. Tukatibu vidonda vya wananchi. Mimi nimefanya kazi ya mahusiano ya jamii. Miradi yoyote itakayokwenda kutekelezwa na Serikali kwa wananchi wenye vinyongo lazima ikwame! Twendeni tukatibu magonjwa. Kuna watu 50 hapa wamepita bila kupingwa kwenye Majimbo, wapo humu! Miradi mikubwa imeelekezwa kwenye majimbo yao unategemea utekelezwaji wa miradi ile utakwendaje? Lazima tutoe vinyongo, watu waseme tuyamalize. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe mwenyewe unajua… kumtangaza Bwana mdogo pale ilibidi waniweke jela, nina kinyongo…. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Spika, muda wako umeshaisha, muda wako umekwisha.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja hizi mbili za Kamati.

Mheshimiwa Spika, naomba ni-declare kwamba mimi ni mdau mkubwa sana wa mazingira; lakini ukiacha hivyo, hapa Bungeni mimi ni mdau mkubwa sana wa meno ya tembo, ninayetetea tembo wasing’olewe meno.

Mheshimiwa Spika, nimeguswa sana na mjadala unaoendelea nchini juu ya hili suala la Ngorongoro. Labda nishauri kabla sijaendelea, ipo haja kubwa ya Wabunge kutembelea hifadhi zetu. Mimi ni mdau mkubwa sana. Ipo haja kubwa ya kuzitembelea ili tuone tunapokuwa tunazizungumzia tunamaanisha nini? Najua hilo unaliweza, utupeleke tukazitembelee hizo hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 1979 Hifadhi ya Serengeti na Hifadhi ya Ngorongoro zilipewa hadhi ya Urithi wa Dunia; siyo wa Tanzania, ni Urithi wa Dunia. Mwaka 2018 UNESCO iliipa hadhi Ngorongoro kuwa ni moja kati ya Eneo la Utalii wa Miamba (Global Geopark), Aprili, 2018.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, hadhi hii haitolewi ovyo ovyo. Afrika hadhi hii ya Geopark iko kwenye nchi mbili tu; ipo kwenye nchi ya Tanzania na Morocco. Ni nchi mbili tu kwa Afrika. Yaani duniani ziko nchi tano tu zenye hadhi hii; zinaongezeka Brazil hapo na nchi nyingine. Kwa hiyo, ni nchi tano tu zina hadhi ya kuwa na utalii wa miamba, moja kati ya nchi hizo ni Tanzania kupitia Ngorongoro Park. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tangu tumepewa hadhi hiyo mwaka 2018, ndiyo ile aliyokuwa anasema kaka yangu pale, ndiyo kwa mara ya kwanza Tanzania tuliweza kuingiza mapato ya nchi shilingi bilioni 148 kwenda shilingi bilioni 150 baada ya kupewa hadhi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kupanga ni kuchagua. Tanzania ni nchi kubwa sana, tuchague lile eneo liwe la makazi ya watu au liwe moja kati ya Urithi wa Dunia, Utalii wa Miamba na chanzo cha tatu cha mapato kwenye nchi hii? Kupanga ni kuchagua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nimekwenda Ngorongoro hivi karibuni. Nimefika pale, hilo eneo ambalo wanasema ndugu zangu wanaishi Wamasai, hali ni mbaya. Wale watu pale wamesema ng’ombe ziko laki moja, siyo kweli, kuna mifugo zaidi ya laki nane iko mle ndani, lakini mifugo inayomilikiwa na wazawa wa pale, wale Wamasai ni asilimia tatu tu. Sasa swali tujiulize, ile mifugo mingine inamilikiwa na nani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkitaka tuweze, Mheshimiwa Waziri Mkuu yuko hapa, toa tangazo kesho kwamba wale wananchi ng’ombe wanazomiliki zote ziwe za kwao, utaona anapigwa mwingine, analia mwingine. Utaona! Zile ng’ombe siyo zote ni za wale Wamasai. Vyombo vya dola si vipo! Au kazi yake ni kutumwagia sisi maji ya washawasha! Si waende wakafanye research pale! Wamasai wale hawamiliki zile ng’ombe wala kondoo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye haya mambo ya uhifadhi, haya mambo kidogo ni ya kitaalam, kibaya kuliko vyote, wale ndugu zetu siku hizi hawafugi ng’ombe, wanafuga kondoo; na kazi ya kondoo ni moja, kwenye uharibifu wa mazingira kondoo ndiyo inaongoza. Yeye akila, hali majani, anang’oa lile jani lote na mizizi yake. Maaana yake ni kwamba lile eneo litaota mmea ambao siyo rafiki kwenye eneo lile. Tunaenda kuua ule uwanda, na kile kivutio cha Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, tena nimesahau, hii shilingi bilioni ninayosema 148 au shilingi bilioni150 iliyozalishwa mwaka 2018, siyo ya Ngorongoro yote kwa ukubwa wake, ni kale ka- crater tu, kale ka-Ngorongoro Crater ndiyo kamezalisha hela zote hizo. Sasa imagine, eneo lote lile lingefanyiwa uwekezaji, kwa sababu crater pale ziko zaidi ya maja; ziko tatu sijui, zote zingefanyiwa uwekezaji, zote zingefanyiwa uendelezaji, nchi hii ingekuwa na fedha kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine watu wanajificha huko kwenu, ni majizi wengine. Yaani wanajificha chini ya siasa kumbe ndio ananyonya Taifa hili halafu mwisho wa siku anasema nawatetea; hawatetei watu, anatetea mali zake ambazo zimetunzwa ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro.

T A A R I F A

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Olelekaita.

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naomba tu nimpe taarifa mzungumzaji kwamba ukurasa wa 37 wa Ripoti ya Kamati, inasema hivi na ninaomba ninukuu: “Serikali imekuwa ikitumia mfumo wa matumizi ya ardhi mseto (multiple land use system) katika Hifadhi ya Ngorongoro kwa mujibu wa sheria na umeiletea Tanzania sifa ya kuitwa hifadhi na sehemu ya Urithi wa Dunia.

Mheshimiwa Spika, nataka nimpe tu taarifa mzungumzaji, wakati Ngorongoro inapewa hiyo hadhi ya Urithi wa Dunia, wafugaji hao walikuwepo na maisha yalikuwa yanaendelea; na sheria inaruhusu.

Mheshimiwa Spika, nampa mzungumzaji taarifa hiyo. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, nimetoa ufafanuzi hapa wa matumizi ya ile kanuni ya kutoa taarifa na ndiyo maana hapa mbele huwa kuna nafasi zinatolewa za Mbunge kuchangia. Taarifa aliyoitoa sijaelewa ni eneo gani la Mheshimiwa Salome, labda ni sehemu ya kwanza aliyokuwa anatoa takwimu au ulikuwa unampa taarifa hiyo kwenye hoja ipi? Kwa sababu mimi nasikiliza ule mtiririko unavyokwenda, yaani hii taarifa uliyoitoa hapa ni kwenye mchango wake upi?

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, napenda tu ku-clarify. Alianza kwa kuelezea Ngorongoro kutambuliwa na UNESCO na kwamba imepewa hadhi ya Urithi wa Dunia. Kwa hiyo, nataka tu nimwambie kwamba Taarifa ya Kamati inasema hivyo na hao watu walikuwepo tu kipindi kile.

SPIKA: Sawa.

Waheshimiwa Wabunge, kabla hujasimama Mheshimiwa Salome; Kanuni ya 77 ngoja nisimame ili tuelewane vizuri. Kanuni ya 77 ndiyo inayozungumza kuhusu taarifa. Ukitoa taarifa sehemu ambayo siyo unayotolea ufafanuzi, unamfanya kwanza mchangiaji asielewe kama apokee taarifa yako ama asipokee. Ndiyo nasema lazima msikilize anapoingia kwenye hoja nyingine. Kwa sababu hapa alishaingia kwenye hoja nyingine ya kuashiria kwamba kuna watu wengine ambao mifugo yao ipo kule na sio wale wakazi wa pale. Kwa hiyo, nilitarajia taarifa inayokuja inataka kuzungumza ufafanuzi kuhusu uwepo wa mifugo ya watu wengine, kwa sababu kwenye hoja ile kuhusu maelezo ya tangazo la UNESCO, tangazo la World Heritage Site alikuwa ameshamaliza akahamia kwenye hoja nyingine.

Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, nawaomba sana, taarifa unatakiwa uitoe pale ili pia hata taarifa zetu Rasmi za Bunge, ziweke vizuri, yaani kwamba kuna Mbunge alisimama akafafanua vizuri ama akampa taarifa Mbunge kuhusu hoja hii. Sasa ikiwa mbali kule, hata sisi huku kwenye taarifa zetu, mtu anakuwa haelewi Mbunge aliyetoa taarifa, ilihusu nini? Kwa sababu kanuni ya 77 inavyoeleza kuhusu taarifa, ni kwamba aidha mtu amesahau jambo fulani au kama hajasahau, basi unataka kufafanua labda kuna jambo yeye hajaelewa.

Nadhani hapo tumeelewa ni wakati gani tutoe hizi taarifa; na kama nilivyosema, leo taarifa nimewaachia mtaendelea kutoa, lakini mzitoe wakati ule unaopaswa ili nasi taarifa zetu Rasmi za Bunge zikae sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, naomba niendelee na mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, nasisitiza, kupanga ni kuchagua, maamuzi yako mikononi mwetu. Sisi kule kwetu Shinyanga ni moja kati ya watu ambao tumeathirika sana na hili suala la kuhamishwa kupisha maeneo ya migodi. Kwanza wamesema vizuri ambao wanawatetea Wamasai waendelee kubaki ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro, kwamba watu hawa miaka ya 1950 walitolewa Serengeti wakaletwa Ngorongoro na walikuwa ni watu 8,000; kwa maana walioletwa ni 4,000 na wale waliokutwa pale 4,000 wakawa 8,000.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi watu wale watu wameshafika laki moja na kitu. Asilimia 64 ya watoto wa wakazi walioko pale hawajui kusoma na kuandika. Utaenda wapi katika nchi ya Tanzania ukute asilimia 64 ya population hawajui kusoma na kuandika? Ilikuwa wakati ule wa Mwalimu Nyerere. Wako pale, wanasema madarasa yapo. Wale watoto hawasomi, kazi yao ni kuchunga ng’ombe za mabeberu ambao wamewapelekea kuchunga kwa ajili ya kuwasaidia kuwapa hela.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Taarifa ya Spika. Taarifa!

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, kesho na keshokutwa twende pale tukatembelee…

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba kuna taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ukisimama na gari la tour, watoto wanakuja kuomba kwenye gari. Ile picha iliyopo kwenye gazeti siyo ya uwongo.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba kuna taarifa kutoa kwa Mheshimiwa Emmanuel Shangai.

T A A R I F A

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nimemsikiliza Mheshimiwa Salome, anasema kwamba qatoto wengi waliopo Ngorongoro hawapo shuleni, wanachunga tu. Naomba nimtaarifu tu kwamba Tarafa ya Ngorongoro ina shule 30 na watoto wanasoma. Waliofaulu mwaka 2021 ambao Mheshimiwa Mama Samia amewapeleka shule ni zaidi ya watoto 1,000 wako Sekondari.

SPIKA: Sawa. Sasa ngoja…

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, kama anasema kwamba watu asilima 64 hawajui kusoma na kuandika, hiyo ilikuwa ni taarifa ya NBS ya 2017 iliyopikwa ambayo ilisema Kata ya Olbalbal wananchi asilima 47 wanategemea...

SPIKA: Mheshimiwa ngoja tuongozane vizuri ili taarifa yako ikae vizuri. Yeye kasema asilimia 64, nawe unakubali kwamba ni kweli isipokuwa ilipikwa. Sasa nitakusamehe kwa sababu ndiyo umekuja, lakini kanuni za humu ndani maana yake unachokisema ni kwamba Mheshimiwa Salome Makamba anasema uwongo; na kanuni zinazozungumza kuhusu Mbunge kusema uwongo ni kanuni nyingine, haiusiki hii ya taarifa. Ukishamtuhumu Mbunge kusema uwongo, tunaanza kufuata utaratibu wa wewe kuleta takwimu nyingine.

Kwa hiyo, ili nikuongoze vizuri utoe taarifa yako vizuri, kama siyo zile 64 wewe unazozijua, ni ngapi? Yaani ndiyo unaweza kusimama kwa kifungu hicho cha taarifa nilichoelezea. Yaani wewe unasimama unasema siyo 64 ila ni hizi.

Kwa mfano, sasa hivi hapa umesema watoto 1,000 wamefaulu. Swali litakuja, watoto 1,000 kati ya wangapi? Kwa sababu ndiyo utoaji wa taarifa. Yaani hapa ukisema 1,000 ukaniambia mimi ni asilimia 100, hilo linakuwa limeisha, kwamba watoto wamefaulu na wako shuleni kwa asilimia 100. La sivyo, tunaanza kuulizana sasa maswali ya kitakwimu hapa halafu tunaweza kuwa hatuna. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, nadhani tunaelewana vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Shangai, ulikuwa umemaliza? Nilikuwa nakuongoza ili taarifa yako itoke vizuri.

(Hapa Mhe. Emmanuel L. Shangai aliinama kuashiria kukubali kwamba alimaliza kutoa taarifa yake)

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kutuongoza vizuri. Kwanza Mbunge aliyekaa anasema anazidi kudhihirisha tu kwamba population ni kubwa. Yaani watu walioko pale ni wengi kuliko wale 8,000 waliotegemewa, waliotungiwa hiyo sheria anayosema Mheshimwia Olelekaita. Sheria ilitungwa kwamba wakae 8,000 kwa sababu it was manageable, lakini sasa hivi hali ni mbaya. Kwa mujibu wa NBS, asilimia 50 ya wakazi wa Ngorongoro ni masikini. Sasa hao unaosema asilimia 50 ni masikini halafu kuna mifugo laki nane, wanakuwaje masikini na watu wana ng’ombe laki nane? Yaani ukiangalia tu hizi data unaona kabisa hapa kuna watu wachache wamepeleka mifugo yao ndani ya hifadhi ambao wanatetea maslahi yao binafsi, wameachana na maslahi ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndani ya eneo la Ngorongoro ni very potential na kuna nchi jirani ambayo pia kuna vita ya kibiashara kwenye utalii. Juzi nimemwambia Mheshimiwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, ziko NGOs ambazo zimesajiliwa, ziko ndani ya nchi hii zinafadhiliwa na nchi Jirani; headquarter ni nchi Jirani. Ukienda kwenye NGO, wote wanaongea lafudhi ya nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ngorongoro ni yetu sote. Serikali ije na mkakati siyo kuwapiga watu mabomu, siyo kuwahamisha watu kwa nguvu. Hawa watu waandaliwe, wajengewe nyumba, wajengewe shule, Kituo cha Afya, wajengewe miundombinu ya kutosha, wahamishiwe pale na wenyewe waishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, amesema vizuri ndugu yangu kwamba ndiyo maana hujaona Masai aliyevaa lubega amekuja hapa kuandamana kwamba hawataki kuhama. Nami nimeenda kwenye hifadhi, wale watu wapo ambao wameomba kwa barua, wameandika wanaomba kuhamishwa kwenye Hifadhi ya Ngorongoro. Wapo! Hata kesho Serikali itangaze, anayetaka kuhama Ngorongoro, uone kama watu hawajajitokeza! Wale watu wanaishi kwenye umasikini wa kutupwa. Watoto wao hawasomi, hao matajiri wenye ng’ombe na kondoo, ziko biashara.

Mheshimiwa Spika, pale Hifadhi ya Ngorongoro imeripotiwa; ukienda kusoma ripoti ya Ngorongoro, mwaka 2021 peke yake tembo zaidi ya 20 wameuawa na faru mmoja. Chanzo cha kifo cha tembo wale na faru ni sumu. Wanawekewa sumu na wakazi wa pale; au wanawekewa sumu na watu ambao ni adui wa tembo na adui na faru. Tunahitaji tuambiwe na nani ili tujue kwamba Hifadhi ya Ngorongoro ni urithi wetu? Tunahitaji tuambiwe na nani ili tujue kwamba Hifadhi ya Ngorongoro ni utajiri wa dunia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakubali, inaweza kuwa yapo maslahi, lakini maslahi ya Taifa yanakuja kwanza. Hakuna mtu ambaye hapendi kuishi vizuri, hakuna! Pia hakuna mtu anayeweza kukubali kuona anazaa watoto hawajui kusoma, hawajui kuandika na mwisho wa siku anaishi kwenye umasikini. Kuna nyumba gani pale Ngorongoro? Nyumba wanazokaa, kwanza sheria haitaki waezeke zile nyumba kwa bati. Kwa hiyo, wanakaa kwenye nyumba ambazo zimewezekwa kwa manyasi. Leo Mbunge anasimama ndani ya Bunge hili anatetea watu wakakae kwenye nyumba za nyasi, mbona yeye hakai kwenye nyumba za manyasi? Kwa sababu Sheria ya Ngorongoro haikubali kujenga nyumba ya bati, yenye mbona anakaa kwenye nyumba nzuri ambayo imeezekwa vizuri! (Makofi)

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Salome kwa sababu nilikusudia kukuongeza dakika moja ya kuchangia, Mheshimiwa Ole- Sendeka.

T A A R I F A

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKE: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe taarifa dada yangu mpendwa Mheshimiwa Salome. Ngorongoro katika Wilaya zote za wafugaji ndiyo inayoongoza kwakuwa na wasomi wengi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; ni Ngorongoro ndiyo iliyomtoa Jaji wa Kwanza Mmasai ambaye ameteuliwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Juzi; ni Ngorongoro ndiyo ina Ph.D. holders wengi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania… (Kicheko/Makofi)

MBUNGE FULANI: Ng’ombe wa nani? Ng’ombe wa nani? Ng’ombe wa nani? (Kicheko)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Ole-Sendeka. Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, hii ni sehemu ya mkakati. Wanachokifanya sasa, wale watoto wakibahatika wakapenyapenya wanaambiwa mkasome sheria ili wakija kule ndani watetee wasitoke kule ndani. Ni sehemu ya mkakati, yaani hii ni sehemu ya mkakati. Waangalie Wamasai wengi waliotoka kule kwanza wana ufadhili, lazima wapate ufadhili wa kwenda Chuo Kikuu. Anayemfadhili nani? Mimi sijapata mfadhili, natoka Shinyanga. Akipata mfadhili, condition namba mbili ni lazima akasome sheria ili kusudi aje akapambane nao. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, najua Serikali ina vyombo. Hii ni sehemu ya mkakati. Naomba Serikali ije na mpango wa kuwahamisha wananchi wanaoishi maisha ya kimasikini ya wanaoishi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro na mpango huo ujumuishe hawa watu kujengewa nyumba nzuri, wapewe ardhi nzuri ya ufugaji na pia wawekewe miundombinu mizuri ya kutosha ambayo itawafanya waishi kwa raha.

Mheshimiwa Spika, juu ya yote, Serikali itangaze, wale Wamasai zile ng’ombe kuanzia leo ziwe zao. Hilo ndiyo litakuwa mwisho wa matatizo. Ng’ombe, kondoo, mbuzi, ziwe za wale Wamasai wa mle hifadhini. Nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hotuba hii muhimu na nitaanza hotuba yangu kwa kumnukuu Waziri wa Fedha kwenye hotuba yake ukurasa wa 72 kwa maandisha makubwa kabisa alisema; “kodi ni jambo la nchi, kodi ndio maendeleo ya nchi yetu” na mimi namuongeze kwa mwanasiasa nguli duniani alisema; “what’s the government gives it must first take away.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachomaanisha ni kwamba ili Serikali iweze kukusanya kodi ni lazima itengeneze walipa kodi wapya na sio kuongeza vyanzo vya kodi kwa walipa kodi wa zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasisitiza maneno yangu hayo kwa kumpongeza Waziri wa Fedha kwenye baadhi ya maeneo ametusaidia kuchechemua na kutengeneza walipa kodi wapya hasa katika eneo la kuweka mikopo na ada bure kwa wanafunzi wa vyuo vya kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema kweli hilo ninampongeza sana kwa sababu moja kati ya changamoto kubwa katika Bunge hili tumeingia tuliokuwa tunapigania sisi tuliokuwa Wajumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii ilikuwa ni kuwapatia mikopo hawa mafundi au technicians au watu wenye ujuzi wa kati kwa sababu kimsingi watu hawa ndiyo wanaajirika kwa haraka, kimsingi watu hawa ndiyo ambao fani zao zinauhitaji mkubwa kwenye dunia ya sasa hasa Tanzania hii ambayo tunaenda kwenye viwanda vidogo vidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme ninaipongeza Serikali kwa upande huo lakini ninao ushauri mdogo. Kwanza wameondoa ada kwenye baadhi ya vyuo kwamba kwa wale wanafunzi ambao watachaguliwa na Serikali kwenda kwenye vyuo vya kati lakini pili wameweka course za vipaumbele kwa watu ambao watapewa mikopo hii na tatu wanasema kwamba wataanza kuwapa mikopo wanafunzi watakaoingia Mwaka huu wa Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani wanasema maendeleo yanapaswa kuwafuata watu na siyo watu kufuata maendeleo. Imekuwa ni utaratibu au desturi Watanzania tunaenda tunavamia mahali, tunajenga nyumba ndiyo Serikali inakuja tunataka tufanye upimaji, urasimishaji na nini. Hao wanafunzi walioanza vyuo vya kati kipindi cha nyuma siyo kosa lao. Serikali haikuwa na mkakati madhubuti wa kuhakikisha kwamba watu hawa wanapata mikopo na wanapata elimu katika mazingira sawa na wale walio katika vyuo vya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme viwekwe vigezo ambavyo vitaweza kuwafaa wale wanafunzi ambao tayari wapo kwenye masomo na hawapati mikopo na viwekwe vigezo kwa wale ambao wataanza ili wote kama Watanzania waweze kunufaika na rasilimali hii ndogo ya Taifa letu ambayo tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee kwa kusema kwamba Serikali lazima itoe ili iweze kuvuna. Huwezi kumkamua ng’ombe ambaye hujamlisha. Serikali imeweka nyenzo kwenye Sheria ya Manunuzi mwaka 2016 kwamba kwenye manunuzi yote yanayofanywa na Serikali itahakikisha 30% ya manunuzi hayo wanapewa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu lakini fursa hiyo imepokwa tena na Serikali kwa upande mwingine unasema hayo makampuni ambayo yatamilikiwa na wanawake au vijana au watu wenye ulemavu ili wapate kuzipata fedha hizo ni lazima waungane kwenye vikundi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kampuni is a legal person yaani anatambulika yeye mwenyewe kama kampuni na ana address yake, ana uwezo wa kushtaki na kushtakiwa, kwa nini unamlazimisha akae kwenye vikundi? Fedha za vikundi zipo kule halmashauri na Serikali inatengenezea mpango. Huu ulikuwa ni mkakati mwingine wa Serikali kuwainua wanawake wenye mitaji midogo na ya kati na ya juu waweze kufikia kufanya biashara na Serikali na Serikali ndiyo mfanyabiashara mkubwa duniani kote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niengomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha busara itumike, marekebisho yafanyike. Kampuni lolote ambalo linamilikiwa na mwanamke kwa 51% au inamilikiwa na kijana kwa 51% au mtu mwenye ulemavu iweze kuwa na sifa kamili bila kulazimika kuungana na makundi mengine kuweza kupata hii mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye jambo lingine la muhimu sana la upandaji wa vifaa vya ujenzi. Hii imekuwa dhana na nimesema hatuwezi kuendelea kama Taifa kama tunaongeza kodi katika maeneo mbalimbali badala ya kuongeza walipa kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna tatizo la msingi hapa. Serikali mwaka jana iliongeza kodi kwenye nondo, ikaongeza kodi kwenye mabati,Mwaka huu imeongeza kodi kwenye cement. Hivi mnataka tukakae kwenye nyumba za udongo? Mimi nataka kujua. Nalielewa lengo la Serikali, sekta ya cement, sekta ya nondo kwa maana ya chuma, ya mabati ni sehemu ambayo inabiashara kubwa sana lakini tusiwasahau Watanzania wa kawaida ambaye anatumia rasilimali hizi kujiboreshea mazingira yao ya kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mifumo yake ambayo inaweza kujua manunuzi haya yanafanyika kwa ajili ya viwanda, kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu na manunuzi haya yanafanyika kwa ajili ya wananchi kuboresha mazingira yao ya kuishi. Serikali imetueleza hapa juzi wanasema wenyewe wanayo Electronic Tax Stamps wanatumia mfumo wa kielektroniki kwa ajili ya kuweza ku-track. Kwa nini Serikali isitumie mfumo huo huo wakamuongezea tu huyu mkandarasi hadidu za rejea kwamba mabati, cement, nondo ambazo zinatumika kwa ajili ya ujenzi wa madaraja, barabara sijui viwanda hayo yawe na tax yake tofauti na yale material yanayotumika kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za kawaida? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi cement iuzwe leo shilingi 16,000 Dar es Salaam, Shinyanga inafika kwa shilingi 30,000. Angalia leo bati la grade 30 unaenda kuliongezea gharama. Mtu wa kiwanda hatumii bati la grade 30 lakini ikipunguziwa kodi wananchi wataacha kuezeka na nyasi kule kwangu Shinyanga. Nondo ambazo zinatumika kwa ajili ya matumizi ya nyumbani ni millimeter 10, millimeter 12. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anaweza tu kusema wale watu wanaohusika na electronic taxation waweke hizo stamp. Zile zinazotumika kwa ajili ya domestic ziwe na gharama zake na zinazotumika kwa ajili ya industrial ziwe na gharama zake waongeze kodi huko lakini huku kwa wananchi kwa ajili ya kuboresha mazingira ya wananchi, kwa ajili ya kuboresha makazi na tulishasema tangu Azimio la Arusha. Mwalimu Nyerere alisema tuna ujinga, umasikini mpaka leo tunahangaikia kweli makazi wananchi sehemu nzuri ya kukaa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuhangaika na hilo, niseme niiombe Serikali kwenye eneo la kuongeza kodi kwenye vifaa vya ujenzi tunawaumiza Watanzania wa kawaida. Tunawaumiza Watanzania wa kawaida kwa hiyo tutofautishe tuweke madaraja na vifaa vya ujenzi ikibidi vitolewe bure. Wakati tunazungumzia hapa biashara ya cement na bei ya cement, tafiti zilizofanyika za haraka haraka cement Tanzania inaweza kuuzwa kwa shilingi 10,000 kwa mfuko lakini sasa hivi ukienda Mwanza cement ni shilingi 28,000. Leo tumeongeza kodi haya umetoa kwenye kodi ya cement umeongeza bado unaongeza kwenye kodi ya mafuta umeongeza shilingi 100, maana yake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo cement kule imeshaongezewa gharama kuisafirisha mwisho wa siku anayeathirika ni mlaji. Umeshaiongezea gharama kuisafirisha kutoka Dar es Salaam ikifika Shinyanga imepanda bei zaidi msafirishaji anakwambia gharama ya mafuta imeongezeka wala haibebi gharama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana sana Serikali inayo mifumo tena mizuri ya kielektroniki ambayo inaweza ku-trace matumizi ya vifaa hasa vifaa vya ujenzi hivi ni kwa ajili ya domestic na kuboresha maisha ya Mtanzania, hivi ni kwa ajili ya maendeleo na ujenzi wa miundombinu watofautishe matumizi hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho niongelee kuhusu bakaa. Mheshimiwa Rais anajitahidi sana kutafuta fedha kwa ajili ya miradi mbalimbali ya kimaendeleo. Kwa sasa nahudumu kwenye Kamati ya TAMISEMI. Bakaa fedha ambazo zinabaki yaani halmashauri zipo zinazoomba fedha hazipelekewi, zipo ambazo zinaomba fedha kidogo wanapelekewa fedha zaidi, zipo ambazo zinapelekewa fedha ya kutosha haitumii mpaka mwaka wa fedha unaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, ningeiomba Serikali kwa kweli na hili liko kwenye dhana ya utawala bora na kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri nimeliona. Ningeomba Serikali kwa nia ya dhati kabisa kila mtendaji apimwe kwa kazi anazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kukubali tunakwenda kwenye halmashauri kukagua unakuta Mkurugenzi ana fedha kwenye account, miradi haitekelezwi ukimuuliza anasema eti kamati haijakaa hatujakaa kujadili na kufanya nini, mara sijui mifumo haifanyi kazi. Kila mtu apimwe kwa utekelezaji wa kazi zake na sasa hivi tunavyoelekea mwishoni mwa mwaka, tathmini ifanyike ni Mkurugenzi yupi ambaye ameshindwa kutumia fedha kwa makusudi, ni yupi anafanya kwa uzembe, wengine hawawalipi wakandarasi kwa sababu wanajua itatengeneza riba ambayo na yeye atakuwa ni mnufaika kwneye riba hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Serikali kwenye eneo hili la bakaa ni eneo ambalo limekuwa ni sumbufu sana kwenye maeneo ya halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule hazijengwi, mabweni hayajengwi, miradi haitekelezwi ukiuliza anakwambia mara mifumo, kamati haikukaa, sijui force account haifunguki. Sisi hatutaki maelezo, it is either ufanye kazi kwa ajili ya Watanzania au useme umeshindwa aje mwingine atusaidie kutekeleza majukumu hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, natamani niwe na neno zuri la kumwambia Mama yangu Balozi Mulamula, lakini labda nianze kwa kusema unahitaji kufanya usafi kwenye nyumba yako, unahitaji kusafisha Wizara ya Mambo ya Nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mama Rais Samia Suluhu Hassan amejipambunua kutangaza Sera ya Mambo ya Nje, amejipambanua kwa kutangaza diplomasia ya uchumi katika nchi yetu. Na kwa kufanya hivyo ameona tofauti na watangulizi wake ana uwezo mkubwa wa kutuletea maendeleo Watanzania kupitia mahusiano na mashirikiano mazuri na mataifa mbalimbali hapa duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu hiyo, vipo vikwazo vingi ambavyo wewe kama balozi mbobezi ni lazima uviondoe ili kuweza kuifanya dhamira ya Mama Samia Suluhu Hassan iweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tulikwenda Dubai, Marekani, tumefanya Royal Tour, tumeita wawekezaji, lakini kwa mfano Mkataba wa Kimataifa wa Huduma na Biashara ambao tuliingia mwaka 1994 mkataba ule unaruhusu wawekezaji kutoka nje kwenye maeneo mawili tu; eneo la utalii na usafirishaji kwa maana ya eneo la utalii na eneo hoteli kuanzia ngazi ya nyota nne. Sasa jiulize nguvu tunayotumia kutangaza, lakini kwenye eneo hilo la huduma tumeridhia kwenye maeneo haya mawili tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia tena mama yangu unakazi kubwa sana ya kufanya alignment ya sheria zetu, ya kufanya alignment ya mikataba mbalimbali ili wawekezaji waweze kuja kama ambavyo Rais wetu anawaomba na kuwasisitiza waje kuwekeza kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwekezaji yeyote duniani niliwahi kusema hii kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara na leo narudia kwenye Wizara hii ya Mambo ya Nje, mwekezaji yeyote ambaye anatumia pesa zake kuja kuwekeza ndani ya nchi ni lazima afanye kitu kinaitwa economic intelligence lazima afanye intelligence. Hivi tunavyozungumza tunakwenda kuwatangazia kule lakini wanajua Shinyanga kunapatikana dhabahu na almasi, wanajua Arusha Mererani kunapatikana Tanzanite wanajua rasilimali tulizonazo, lakini kitakacho wakwamisha ni sheria zetu, mikataba yetu, tamaduni zetu na namna ambavyo tunakosa msimamo kwenye mazingira ya kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikutolee mfano, mwaka 2019 tulipitisha sheria mbili humu ndani zinasema sisi Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tutakuwa na uwezo wa kuitisha mikataba ya wawekezaji na kuipitia mikataba ile na kama hiyo mikataba itaonekana kwamba haiwanufaishi Watanzania kutokana na rasilimali zao mikataba ile inaweza kufanyiwa marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kwa clause kama hiyo ni nani anaweka kuja kuweka hela yake hapa, yaani kuna vifungu vya namna hiyo kwamba mtu anaweza akaingia mkataba akijua tumeshasaini deal, tumeshafunga mkataba lakini kesho asubuhi anaibuka Rais mwingine tofauti na Rais ambaye alikuwa labda ana nia njema anasema huu mkataba namna ulivyopitishwa pitishwa huu lazima tuufanyie review, tunafanyia review mwisho wa siku mkataba unabadilika ni unstable business environment. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa sababu hiyo ndiyo maana hata unaona Mheshimiwa Waziri hicho kifungu hakitekelezeki, kwani tumeomba mara ngapi ilete mkataba hapa hakitekelezeki kwa sababu yaani haiwezekani ku-review mikataba kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nchini tuna kitu kinaitwa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, tena kwa bahati nzuri Mahakama hiyo ipo Arusha hapa hapa Tanzania. Mheshimiwa Waziri unaomba fedha bilioni nne kwa ajili ya ujenzi wa mahakama na bilioni 1.2 kwaajili ya uendeshaji wa mahakama. Hakuna mtanzania au taasisi ya Tanzania inayoruhusiwa kwenda kufungua kesi kwenye ile mahakama na mwaka 2019 ndiyo tulijitoa kwenye haki hiyo.

Sasa mama yangu Mheshimiwa Liberata Mulamula utusaidie hii foreign policy na hii economic diplomacy anayoitangaza Mheshimiwa Rais inatokana na msimamo mzuri msimamo ambao una tabirika wa kibiashara ndani ya nchi mpaka mtu aje kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wamesema vizuri ndugu zangu hapa kuhusu suala la uraia pacha, tumeenda kuwavutia wawekezaji na baina yao ni Watanzania wanaoishi nchi za nje, tunasema waje kuwekeza, lakini unasema kwasababu anakaa nje nchi hawezi kuja kuwekeza huku ndani na kumiliki ardhi kwa sababu ni foreigner. Sasa mmoja ametoa taarifa anasema kuna kitu kinaitwa hadhi maalum, ni nini hiki hadhi maalum ni kitu gani? Kwa nini msiseme tunaposema hadhi maalum tunaamanisha itakuwa moja na mimi nilitegemea hivyo na ndiyo maana sikuhoji Mheshimiwa Rais aliposema kwamba watapewa hadhi maalum kwa sababu nilijua Mheshimiwa Waziri ukija kusoma hotuba yako utafafanua nini maana ya hadhi maalum na hilo ndilo swali la Watanzania wengi, na umesema vizuri wanachangia kwenye Pato la Taifa lakini ninani atakayekubali kwenda kuwekeza kwenye nchi ambayo hana uhakika kama mali anayoenda kuwekeza pale ataendelea kuwa nayo vizazi na vizazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Hawa watu wanafanyakazi ngumu diaspora, mimi nakuomba unapokuja kuhitimisha hapa uje utuambie hiyo inayoitwa hadhi maalumu ni kitu gani hasa humo ndani kuna vitu vya namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu mwanzoni Waziri wetu wa Mambo ya Nje alipeleka ripoti ya utekelezaji wa haki za binadamu ambayo ni nzuri sana, mimi nakubaliana nayo, tume-adopt mambo mengi sana na moja kati ya jambo ambalo tulili-adopt tumesema hivi naomba ni quote; “The State supports the part of recommendation which leads to take all necessary measures to combat discrimination and violence against women including domestic violence” halafu mkaenda kukiri mkasema; “The State notes that part of the recommendation of on the family violence are this concept is yet to be define in the state policies” yaani sera zetu za nchi hazitambui au hazija accommodate suala la unyanyasaji (domestic violence) kwenye ngazi ya familia tumekubaliana nalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wewe unaona kwenye vyombo vya habari, jana kuna mwanamke Mwanza ameuwawa, leo tunaona hapa wamechangia vizuri sana wenzangu kwenye bajeti zao, watu wanauwawa, wanawake wanauliwa kwenye familia zao. Shinyanga asilimia 56 ya watoto wa Shinyanga wanaolewa wakiwa wadogo wanapata mimba za utotoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii ni UN Report imepelekwa na Mheshimiwa Waziri anahusika, ndiyo mwenye dhamana ya hii ripoti yetu, ndiyo maana namwambia anatakiwa kusafisha nyumba yake. We have a lot of International Agreement ambazo hatuja ratify. Zipo International Agreement ambazo hatuja domesticate, hii yote ndiyo msingi, ndiyo tija, ndiyo shibe ya hiyo foreign policy ambayo Mama Samia Suluhu Hassan anahangaika kutembea duniani mama wa watu anamiaka sijui sitini na ngapi kuhakikisha kwamba anavutia wawekezaji. Sheria zetu, mipango yetu, mikataba yetu kama haiwalindi wawekezaji ndani ya nchi tutazunguka sana na jambo hili litakuwa ni la muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimalizie fedha tunayoenda kuwekeza kwenye African Court Peoples and Human Rights kama nimei-quote vizuri ni fedha nyingi, tufungue, kuna wakati mwingine haya mambo mnayafunga watu wanadhania kwamba mna nia mbaya yaani yanaonesha tu kwamba kuna dhamira ovu kwenye kufunga watu wasiende na taasisi, ruhusuni watu waende kwenye hizi mahakama rudisha kile kifungu cha 38 ili article tuliyo withdraw 38(6) nafikiri, rudusheni twende kwenye mahakama hizo tufungue, sisi ndiyo host na by the way umeomba fedha kwaajili ya kuendeleza mahakama hii, kwa nini unakataza wanachi wa Tanzania wasiende kushtaki kwenye mahakama ile, naelewa mazingira ya kisiasa yalivyokuwa mwaka 2019 wakati tunajiondoa, lakini mmejinasibu wenyewe kwamba huko tumetoka. Sasa hivi tuna uhuru wa vyombo vya habari, sasa hivi tuna uhuru wa waandishi, sasa hivi tuna uhuru wa watu kusema na mambo kama hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ni hivyo na hiyo mahakama ndiyo kazi yake kwenda kusikiliza watu wanaonyanyaswa waandishi wa habari, kwenda kusikiliza watu wanaonyanyaswa kwaajili wameongea na freedom of assembly, fungueni watu waende nchi ifunguke kama mnavyosema lakini tukisema tuna advocate, tunatangaza Tanzania ifunguke kiuchumi ilihali tunajua kabisa hapa yaani tunasema nini tunajipiga ngwala wenyewe, Mheshimiwa Liberata safisha nyumba yako, usimkwamishe Mheshimiwa Rais hatutaki kurudi kwenye kukusanya shilingi 20,000 za machinga. Mama analeta matrilioni ya fedha barabara zinajengwa, analeta matrilioni ya fedha vituo vya afya vinajengwa, biashara ya kuchangisha watu masikini tuachane nayo, fedha kwa ajili ya nchi zinaoendelea huko nje zipo kibao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana. (Makofi/Kicheko)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nianze utangulizi wangu nikijikita sana kwenye Mambo ya Nje. Dunia iligundua kwamba kuna nchi zina nguvu sana. Tuki-apply dhana ya sovereignty of the state kuna baadhi ya nchi inaweza ikaziumiza nchi nyingine. Kwa msingi huo, ikaja dhana ya kidiplomasia, kwamba hawa watu watatumia ushawishi, uwezo, mahusiano kuweza kufanya nchi hizi ziweze kuishi na kufanya kazi pamoja.

Mheshimiwa Spika, nimetoa utangulizi huo kufuatia mambo yanayoendelea kati ya Tanzania na Marekani. Secretary of the State alitoa kauli kuhusu mwenendo wa nchi yetu kwenye mambo ya demokrasia, haki za binadamu na mambo mengine. Akaeleza, tusipokuwa makini, tunaweza tukaharibu mahusiano yetu na Marekani na matokeo yameanza kuonekana.

Mheshimiwa Spika, sasa anapotokea Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi yetu anajaribu ku-confront statement ya Marekani kwa kutishia kwamba watatufanya nini na tukitaka tutarudisha watu wao. Hiyo siyo diplomasia na huo siyo msingi wa diplomasia duniani.

Mheshimiwa Spika, hili narudia. Tuliposema tunahitaji Waziri wa Mambo ya Nje aliyebobea kwenye diplomasia, tulimaanisha mtu mwenye ushawishi, mtu mwenye uwezo wa kuimarisha mahusiano ili Tanzania, nchi masikini tuweze kuimarika kiuchumi na kuweza kutekeleza bajeti zetu kupitia donor community. Sasa hili inabidi tuliangalie kwa umakini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka jana, 2019 mwishoni, Tanzania iliyopewa heshima ya kuwa Makao Makuu ya the African Court on Human and People’s Rights tumetishia kama siyo kujitoa, maana zimetoka kauli mbili za Mawaziri. Mheshimiwa Prof. Kabudi anasema tumejitoa, Mheshimiwa Mahiga anasema hatujajitoa, tumeomba wabadilishe protocol.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu iliyopewa tangu enzi za uhuru, AICC hapa Tanzania, tuna hii Mahakama ya Afrika, siyo kwa bahati mbaya. Kwa hiyo, kusema tunajitoa kwenye AICC, kusema tunataka kujitoa kwenye the African Court on Human and People’s Rights, ni kujaribu kuona ile heshima tuliyopewa hatukustahili.

Naiomba Serikali, tunayo haja kubwa ya kuimarisha diplomasia katika nchi yetu. Hili siyo jambo la kufanyia mizaha kwa sababu kurudisha heshima tuliyopewa, zipo nchi nyingi sana zinajaribu na wamekosa fursa hiyo.

Mheshimiwa Spika, niseme kidogo kuhusu ndugu zetu walioko China, waliopata ugonjwa wa coronavirus. narudia tena, kazi ya kwanza ya Serikali ni kulinda, kuhudumia na kuhakikisha watu wake wapo salama. Sasa leo Mbunge anasimama Bungeni, anauliza swali mahususi: Tanzania itafanya hatua gani kuhakikisha watu wake wanarudi nchini salama? Serikali inasema, watu wabaki huko huko kwanza, haya mambo mengine tutashughulikia pole pole.

Mheshimiwa Spika, hili Bunge ni la wananchi. Serikali kazi yake ni kulinda ustawi wa wananchi na kulinda usalama wa wananchi. Tunahitaji kauli thabiti ya Serikali kuhusu evacuation process.

MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Salome, kuna taarifa.

MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Nimekuona Mheshimiwa.

T A A R I F A

MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba tu nimkumbushe Mheshimiwa Salome kwamba tamko la kusema raia wa Tanzania ambao wapo nchini China ilikuwa ni kwa manufaa yao. Tumeshuhudia Serikali ya China ikiwashauri wananchi wao wenyewe wa Jamhuri ya Muungano wao wa China waendelee kukaa ndani kutokana na maambukizi au mfumo wa maambukizi wa ugonjwa ule. Kwa hiyo, kubaki kwao ndani kuweza kufanya movements za kutoka kwenye miji yao kuja mpaka Tanzania kunawaweka kwenye hatari zaidi kuliko kuendelea kuwa china.

Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Salome, pokea ushauri huo.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika kwa kulinda heshima ya kiti chako, uliielekeza Serikali hapa wiki iliyopita walete kauli, walete mpango wao wa evacuation kwa ajili ya ndugu zetu wanaoishi China. Leo ni Jumatano, watu wetu wanaishi kwa hofu, wazazi wao walioko Tanzania wana hofu. Hivi hii ni serikali gani isiyojua hili? Tumeelezwa kwamba Marekani wameshaanza evacuation process, watu wanarudishwa, Ujerumani wanarudisha watu Tanzania…

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Tanzania watu wetu wanaishi kwa hofu na wale ni Watanzania wenzetu.

SPIKA: Mheshimiwa Salome, kuna taarifa unapewa. Nia ni kukusaidia tu Mheshimiwa Salome kupitia taarifa hiyo. Mheshimiwa Waziri Nchi, tafadhali.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, hatugombani katika jambo hili ambalo lina maslahi ya Watanzania na nchi kwa ujumla. Kwa hiyo, Mheshimiwa Salome ajue kabisa kwamba hatugombani katika jambo hili.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka ndani ya Mkutano huu wa Bunge Mheshimiwa Waziri Mkuu hapa alishatoa maelezo, lakini Waziri mwenye dhamana ya Wizara ya Afya alishatoa maelezo yakinifu. Sasa tunachotaka kufanya hapa kwa muktadha wa jambo hili ambalo ni lenye afya tu, Mheshimiwa Salome anapaswa kushauri zaidi kuliko kulalamika ama kuishutumu Serikali haijachukua hatua zozote.

Mheshimiwa Spika, ili kuthibitisha kwamba Serikali imefanya kazi yake ipasavyo, ndiyo maana Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa tamko, Waziri wa Afya ameendelea kutoa tamko na hiyo yote ni Serikali. Hatulali, tunaendelea kulifanyia kazi jambo hilo. Kwa hiyo, tuko tayari kupokea ushauri, lakini siyo tuhuma kwamba Serikali haijajali wala kushughulikia suala hilo.

SPIKA: Unapokea taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, hiyo taarifa siipokei. Hivi unafikiri Bunge lako linajua Watanzania wangapi wanaumwa? Watanzania wangapi huenda wameshapoteza maisha? Watanzania watarudi tarehe ngapi mwezi wa ngapi hapa nchini? Marekani wamesharudisha watu wao nchini. Hii Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayojitapa ina ndege, itumie ndege hizo nane waweke moja Watanzania warudi nchini kwa maslahi ya Taifa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana. Dakika zako zimekwisha.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …na kwa ajili ya kuleta amani katika nchi yetu. Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie kwenye Wizara hii muhimu ya Fedha na Mipango. Nianze kwa kusema, wakati naanza kuwa Mbunge tuliambiwa maneno yafuatayo: Ukiwa kama Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, la kwanza ni maslahi ya Taifa lako, la pili ni maslahi ya wananchi wako Jimboni kwako, la tatu ni maslahi ya chama chako, na la mwisho ni maslahi yako binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ameinuka leo Mbunge mmoja, tena Mbunge Mwandamizi ndani ya Bunge hili Tukufu akamnukuu Baba yetu wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, nami nimeona tu nimnukuu Hayati Kambarage Nyerere kwenye Azimio la Arusha la mwaka 1967. Alisema kwamba, “ili kuhakikisha kuwa uchumi wa wananchi unakwenda sawa, Serikali lazima iwe na mamlaka kamili juu ya njia muhimu za kukuza uchumi.@ Akaenda mbali akasema, “Mheshimiwa Mbunge anaposimama, (ukurasa wa 11) kuomba barabara, au shule, au hospitali, au vyote; je, Serikali ina mpango gani?” Majibu, anategemea Serikali iseme, anasema, “naye pia jibu ambalo anagependa kupewa ni kuwa, Serikali inao mpango safi kabisa wa kutengeneza barabara au kujenga shule au hospitali au vyote kwa wananchi wa sehemu Mbunge Mheshimiwa huyo na watafanya hivyo kwa kutumia fedha.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunajadili bajeti ya Wizara ya Fedha. Sisi Wabunge moja kati ya jukumu letu kubwa ni kuisaidia Serikali kupata vyanzo vya fedha. Tutafanya hivyo kwa namna yoyote ile ikiwa ni pamoja na kuwaruhusu wananchi wetu kuachia maeneo muhimu ambapo maeneo hayo yataipatia Serikali fedha. Sheria ya Ardhi ya nchi hii Kifungu cha 4 kinasema, ardhi ni mali ya umma na Rais ndio mwenye dhamana; na inaruhusu Rais huyo huyo kuweza kutwaa ardhi ile kwa ajili ya maslahi ya umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunalo eneo letu very potential na nilisema humu ndani, suala la Ngorongoro atapigwa mwingine, atalia mwingine. Ngorongoro kwa mwaka 2018/2019 imeipatia Serikali yetu mapato ya Shilingi bilioni 150. Ngorongoro ndiyo urithi wa dunia. Leo wananchi wa Ngorongoro wanahamishwa kwa namna ambayo Wabunge wengi humu ndani tunaona wivu, wanahamishwa. Anasimama Mbunge anasema, wanateswa, wanaonewa.

Mheshimiwa Spika, ipo haja ya kupima uzalendo wa Watanzania ambao tunawawakilisha sisi humu ndani, tupimwe uzalendo wetu kwenye Taifa letu. Haiwezekani tuungane na raia wa kigeni kulichafua Taifa letu kwa propaganda zinazofanya tushindwe kukuza uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Watanzania tunajuana. Viingereza vyetu vya Rasi Simba, tunajuana. Leo anasimama mwanaharakati eti Mmasai wa Ngorongoro, wa Loliondo, eti mwanaharakati anaongea Kiingereza cha Malkia. Kiingereza cha ndani kabisa yaani, anasema anawatetea Wamasai wenzie wa Ngorongoro. Tanzania ni yetu, tutaachia rasilimali. Kama kwa kufanya hivyo inasaidia kujenga nchi, inasaidia kukuza uchumi, inasaidia kuongeza biashara, inasaidia kuboresha maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 1999 wananchi wa Kata ya Bulyanhulu, Kakola kule, uliko Mgodi leo wa Barrick ambao sasa hivi unaitwa Twiga, walihamishwa kwenye maeneo yao, wakakiri kuhama kwenye maeneo yao. Leo wananchi mwaka 2008, 2010, wananchi wa Mgodi wa Buzwagi ambao leo ndiyo upo mgodi ule walikubali kuhama kwenye maeneo yao. Wengine mpaka leo wanadai fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hali ndiyo hiyo, mimi wananchi wa Shinyanga wamenituma, wanamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, kauli yake aliyoitoa ya kusema anawapa pesa wananchi wa Ngorongoro kwa kuhama, anawajengea nyumba na kuwakabidhi hati, eti mpaka mtu mwenye wake wa tatu atapewa hati tatu, wananchi wa Shinyanga Mwendakulima na wenyewe wanataka hiyo privilege waliyopewa watu wa Ngorongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania ni yetu sote. Haya mambo ya kubembelezana; Mgodi wa North Mara watu waliondolewa pale kwa mabomu. Haiwezekani leo jamii moja ya Watanzania iwe very much privileged, ionekane yenyewe ndiyo kila kitu, propaganda ziendelee kufanyika eti tunawabembeleza watu kupisha eneo ambalo ni potential, ni urithi wa dunia, eneo ambalo ni rasilimali kubwa duniani, siyo Tanzania. Tunawagopa kwa sababu ya propaganda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi wakati najifunza siasa, niliambiwa propaganda hujibiwa kwa propaganda. Hawa wanasema leo eti Mawakili, wanakwenda Mahakama ya ICC kwenda kuishtaki Tanzania kwa kuwapiga watu wanaoenda Ngorongoro, tutapambana nao Mahakamani. Wale watu wa propaganda wapambane nao kwa propaganda. Haiwezeki tukae kimya ardhi yetu inatumika vibaya, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wa Shinyanga na sisi tunataka haki yetu. Wananchi wa Shinyanga, ilifika hatua, Kahama peke yake imekuwa ya nne Kitaifa kwa kuchangia pato la Taifa kwa sababu wananchi wa Shinyanga walikubali kutoka kwenye maeneo ya madini na kuwaachia wawekezaji ambao leo hii tunapiga kelele hapa, lakini ndiyo pesa za watu wa Shinyanga waliyotoa kwenye maeneo yao wameachia nchi inapata kipato. Nasi tunaidai haki hiyo kwa wivu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, wanatoa sababu eti maeneo yale wameyazoea. Wale maeneo wameyazoea walikuwa wanakaa tu na kuchunga ng’ombe. Shinyanga wananchi wa Mwime, Mwendakulima, Chapua, hawana shughuli nyingine yoyote ya kuwaingizia kipato zaidi ya kuchimba dhahabu. Hawana shughuli nyingine. Ukienda Ibadakuli, Bulyanhulu, wananchi wa Bulyanhulu kule Nyangalata, Namba Tatu, Namba Nne, hawana shughuli yoyote ya kuwaingizia kipato. Asilimia 99 ya wananchi wale shughuli yao ilikuwa ni uchimbaji. Kama suala ni maeneo waliyazoea, na sisi tuliyazoea. Hoja hizi ni batili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaposimama ndani ya Bunge hili sisi kama Wabunge, kazi yetu ni kutafuta vyanzo vya mapato. Tumesikia hapa Wabunge wanasema, wale watu walikuwa wananufaika, tumeinua Taifa hili kwa sababu wanawake walikuwa wanapewa asilimia nne, vijana wanapewa asilimia nne, watu wanaoishi na ulemavu wanapewa asilimia mbili. Leo inapunguzwa mpaka asilimia mbili, mbili, moja, pesa nyingine wanapelekewa Wamachinga. Kakeki kenyewe ni kadogo, tunakagombania, watu wengine wanatetea maslahi binafsi kwenye maslahi ya umma, hiyo haikubaliki. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, Sengerema wananchi wanaachia eneo la Sotta Mining, kaya 1,600 mpaka sasa hivi tunavyozungumza wanatakiwa kuondoka, wapishe mgodi bilioni 740. Wao siyo watu? (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, unapokea taarifa hiyo.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, taarifa ya mjomba wangu Mheshimiwa Tabasam Hamis naipokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mustakabali huo, na bahati nzuri wewe ni Mwalimu wetu mzuri sana. Kanuni za Bunge zinakataza kujadili jambo ambalo limeshajadiliwa na mjadala wake ulishafungwa. Mjadala wa Ngorongoro tulizungumza humu ndani, tukajadili na huo mjadala umeshafungwa. Naomba kwa Mwongozo wako suala hili lisisemwe tena, kwa sababu watu wameshakubali kuhama, watu wameshakubali kwenda kwenye maeneo yao mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasisitiza, zile ng’ombe za wale wawekezaji ambazo wameziweka kwenye Hifadhi, wale watu watoe. Nimeangalia kwenye taarifa ya Habari, zile ng’ombe mlizoziweka kwenye malori ni chache mno. Wekeni zile ng’ombe zote zilizoko kwenye Hifadhi ziende na wale watu kule Handeni. Ndiyo utajua, tangu lini Mtanzania wa kuzungumza Kiingereza cha Malkia, eti amekuwa Mmasai wa Ngorongoro, eti amekuwa Mmasai anatetea wananchi wa Ngorongoro! Hiyo haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya issue ya Ngorongoro natumai umeifunga, nami naishia hapo, sitaisema tena. (Kicheko/Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Muda umeshaisha Mheshimiwa. (Makofi)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi. Mimi niseme mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya TAMISEMI na ningependa kuchangia pale alipoishia Mheshimiwa Mwenyekiti wetu wakati anawasilisha taarifa yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama nchi tuna changamoto kubwa sasa hivi tunayoipitia. Tuna janga na si changamoto, ni janga kubwa sana la uharibifu mkubwa wa miundombinu. Hapa hatupepesi macho, changamoto ni kwamba watu wanaohusika na kutengeneza barabara hawajapelekewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi tuko hapa Wabunge tunashauri, kwenye Kamati tulimwita Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kwa nini barabara hazitengenezwi? Changamoto ni fedha, wenyewe wameshafanya tathmini wanataka shilingi bilioni 131 kuweza kukabiliana na changamoto ya barabara zilizoharibika na miundombinu yote ya barabara nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, anayetoa fedha ni Hazina, hapa hayupo Waziri wa Fedha, hakuna Naibu Waziri wa Fedha tutapata wapi haya majibu?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi wametoa shilingi bilioni 21 tu…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge, Serikali ipo Bungeni kwa hiyo usiwe na wasiwasi endelea kuchangia. (Makofi)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilishauri kwenye Kamati aitwe Waziri wa Fedha atuambie tunapata wapi shilingi bilioni 131 kwa ajili ya kutengeneza barabara za nchi hii? Hakuja kwenye Kamati. Nikawa namsubiri nije nimwambie Bungeni, hayupo; sasa nitaenda kumwambia wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kitokee nini ili tujue kwamba kuna dharura? Madaraja yameshakatika, barabara zina mashimo, ajali zimetokea. Juzi Shinyanga pale kwangu Mto Mumbu, mtu amesombwa na maji na mafuriko, amekufa. Tunataka kitokee nini ili tujue kwamba jamani tuko kwenye hali ya dharura? Mheshimiwa Aida anasema kwake Nkasi watu wameshakufa kule, Dar es Salaam watu wanakufa; tunataka kitokee nini? Kazi ya Serikali ni kuwahudumia wananchi na kuhakikisha wako salama. Nchi ipo kwenye janga, iko kwenye changamoto, shilingi bilioni 131 zinatakiwa… (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …mpaka sasa hivi wamepeleka shilingi bilioni 21 tu kwa ajili ya kwenda kutatua hali ya dharura.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na ninatambua mchango mzuri wa Mheshimiwa Salome Makamba. Naomba tu nimpe taarifa kwamba kazi ya utengenezaji wa barabara zilizoharibika katika maeneo mbalimbali kutokana na mvua zinaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kasi yake kwa mfano Dar es Salaam; Kibamba wamepata, Kawe wamepata na maeneo mbalimbali wamepata. Kwa hiyo nimhakikishie tu kwamba pamoja na kwamba kuna uharibifu mkubwa lakini Serikali haijalala inaendelea kufanya matengenezo ya barabara hizo na hali itakwenda vizuri, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana; Mheshimiwa Salome taarifa hiyo unaipokea?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri, mimi naomba utulie tu nikusaidie kwa sababu tuna changamoto. Nina ripoti ya Mheshimiwa Waziri hapa kuja kwenye Kamati anasema, tathmini imefanyika nchi nzima, halmashauri 184 hali ya uharibifu ili tuweze kurekebisha hiyo hali inatakiwa shilingi bilioni 131. Mpaka sasa hivi Serikali imepeleka shilingi bilioni 21 out of 131 unasema nchi kazi inaendelea au ndio hao wakandarasi wazawa mnawakopa hela wanafanya kazi wanaendelea kufilisika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, we have a serious problem sisi kama nchi na tukifanya maigizo well and good, lakini kama jambo limeshatishia uhai wa wananchi, kama jambo limeshatishia usalama wa nchi, kama jambo linatingisha uchumi wa nchi hakuna muujiza. Yaani ni kwamba tukirudi hapa bajeti ijayo mtakusanyaje hizo fedha kwa ajili ya kutengeneza bajeti? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Patrobass Katambi.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri wa Mheshimiwa Mbunge; ni kweli kwamba Watanzania wanapata changamoto kutokana na majanga ambayo yanaendelea. Uhalisia ni kwamba TMA (Tanzania Meteorological Agency) ilitangaza uwepo wa mvua za El Nino, na uwepo wa mvua hizi umesababisha majanga makubwa karibia nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata katika fedha iliyokuwa imetengwa ya bajeti ambayo ilikuwa ni kwa ajili ya dharura tume-burst, kufikia hatua kwamba fedha zile hazitoshi tena kulingana na uharibifu mkubwa ambao umetokea. Kwa hiyo taarifa yangu ni kwamba Mheshimiwa Mbunge ajue kwenye mazingira ya dharura kuna vitu vinaitwa natural catastrophes ambazo ni majanga asilia ambayo hakuna mtu yeyote alipanga mvua za El Nino zitokee. Ikitokea majanga kama hayo nchi yoyote inaweka utaratibu wa kuhakikisha inakabiliana nayo. Kwa hiyo ni majanga wala siyo kwamba ni Mpango wa Serikali inapanga hivyo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana; Mheshimiwa Salome taarifa hiyo unaipokea?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi hiyo taarifa siipokei, nataka tu nimsaidie kaka yangu pale, Mheshimiwa Katambi. Bajeti iliyopita kwenye TARURA waliomba wapewe 1.6 trillion, wakapewa shilingi bilioni 800 na ushee tukatenga. Akaja Waziri wa Fedha akatulaghai kwamba anaiongezea TARURA shilingi bilioni 350. As I speak right now wakili msomi wamepewa shilingi bilioni 89 tu. Ile 800 hawajapewa, tuliyodanganywa hapa wameongezewa 350 hawajapewa, hiyo hela unayosema inaenda kufanya mambo ya natural catastrophes haifiki hata asilimia 10 ya target ambayo tunayo. Sasa si tunafanya mzaha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuchukulie jambo la miundombinu ya barabara kwa udharura wake. Kamati ya Miundombinu, Kamati ya TAMISEMI, Kamati ya Bajeti na Kamati ya Fedha ni lazima tukae tuje na msimamo wa Bunge. Nini kifanyike kutatua changamoto ya barabara kwenye hii Nchi? Watu wameshakufa, ajali zimeshatokea, uchumi umeshatetereka inatosha kulifanya jambo hili kuwa ni jambo la dharura na kuchukuliwa kwa uzito wake. Sisi kama Bunge tuishauri Serikali juu ya jambo hili, unless otherwise sisi tutaonekana tumeshindwa kuishauri Serikali katika jambo hili la dharura, tutaonekana tumeshindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwa wakandarasi wazawa. Mheshimiwa Waziri amekuja na wazo zuri sana la TARURA Samia Bond, lakini nikwambie tu changamoto siyo bond, changamoto ni sheria mbovu ambazo zinawabana wakandarasi wetu wanashindwa kufanya kazi za Serikali. Leo mkandarasi atapata kazi ya kujenga barabara anaambiwa nenda kalete bank guarantee, anaambiwa nenda kalete sijui nini ya benki. Yaani kabla hajaanza kujenga Barabara asilimia 80 ya fedha zake ameenda kuziweka kama bond benki ili aweze kupata guarantee akafanye hiyo kazi; atafanyaje kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naelewa miradi mingi hasa inayotekelezwa kwa fedha za wahisani inakuja na masharti magumu lakini you scratch my back I scratch yours. Kama wanataka kutupa misaada watupe misaada ambayo inatufaa na inayowanufaisha wakandarasi wetu wazawa. Ni lazima tufanye mapitio ya sheria kuhakikisha Watanzania wananufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachi zote zinazoendelea duniani mtaji wao namba moja ni population yao. Population ya Watanzania tumefika milioni 60 na kitu. Tukiwawezesha wakandarasi wazawa angalau watano tu (makampuni matano kwenye kila mkoa) lazima tutoboe, yaani lazima tufanikiwe. Hakuna muujiza kwenye hilo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Salome, muda wako umekwisha.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, Nakushukuru kunipa nafasi nichangie wizara hii ya muhimu ya Katiba na Sheria. Mwaka 2018/2019 kwa niaba ya Wabunge wenzagu wanaotetea haki za mtoto wa kike, nilishika shilingi ya waziri ndani ya Bunge hili nikimtaka waziri kufuata maelekezo ya Mahakama ya Rufaani kuleta mabadiliko ya Sheria ya Ndoa; kwa kubadilisha Kifungu cha 13 na 17 ambacho kina mruhusu mzazi kumuozesha mtoto chini umri wa miaka 18, Waziri alitoa majibu ambayo kwa kweli sikuridhika nayo lakini kwasababu wengi wape, walishinda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mama Samia Suluhu Hassan, amejipambanua kwamba ni mwanamke anayetetea haki, demokrasia, utu na usawa. Namtaka waziri, atekeleze hukumu iliyotolewa mwaka 2017, Kesi Na. 204 kati ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Attorney General. Ambayo mahakama ya Rufaa the sealing ilielekeza ndani ya mwaka mmoja, sheria hii iletwe ndani ya Bunge, Vifungu hivi vifutwe na mtoto wa kike apate haki sawa ya kuamua kuhusu ndoa yake akiwa na miaka 18. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumuozesha mtoto wa kike chini ya miaka 18 si tu inamuhatarisha maisha yake ni unyanyasaji wa kijinsia, kwasababu hawezi kusimama mahakamani kama haitaki ndoa ile iko chini ya umri. Inamletea madhara ya uzazi anaweza kuzaa Watoto njiti, anaweza kupata fistula; walijitetea Serikali kwamba haya ni mambo ya kidini lakini kipekee kabisa nitoe nukuu ya Baraza la Ulamaa lililokaa mwaka 2019 walisema; “Uislamu umezingatia kuwa hili mwanamke aweze kuolewa ni lazima awe tayari kiakili na kimwili. Hatuwezi kuwanyanyasa Watoto wa kike kwa kuwaozesha katika umri mdogo kuna tofauti kubwa sana kati ya umri wa kufanya mapenzi na umri wa kuhimili mikiki mikiki ya ndoa.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namtaka waziri alete marekebisho haya kudhirihishia sisi Bunge tunaheshimu utawala wa Sheria, tunaheshimu Mihimili mingine kwa kutekeleza maelekezo ya Mahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo changamoto kubwa ya Sheria ambayo imetungwa ndani ya miaka mitano. Sheria katika mwenendo wa makosa ya jinai inayohusiana na mambo ya plea bargain yaani kumpa mamlaka Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali kufanya makubaliano na watuhumiwa na kulipwa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipinga ndani ya Bunge hili kuhusiana na sheria hii, kwasababu kwanza; Mahabusu umemuweka ndani, umemuweka kwenye mazingira magumu, amepoteza rasilimali, amepoteza uwezo wa kutafuta fedha, halafu unamuita unamwambia njoo tukubaliane unilipe kiasi kidogo ili nikuachie. Hakuna usawa katika makubaliano hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yalifanyika, ilitekelezwa sheria ile, fedha zikakusanywa kilichotokea kwa mara ya kwanza na cha kushangaza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ilivamiwa na fedha zikaibiwa hatujui ziliibiwa shilingi ngapi! hatujui fedha zilikwenda wapi! Mpaka leo hakuna kinachoendelea wamekaa kimya na hakuna anayewajibika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulifuata Sheria ya Plea Bargain mzizi wake ulikuwa ni Marekani, India waka-adopt mfumo ule, Tanzania tukauchukua tukauingiza Bungeni. Lakini wenzetu walioanzisha Wamarekani waligundua, kwenda ku-negotiate na mtuhumiwa aliyeko mahabusu aliyepoteza kila kitu mpaka utu wake, kwenda ku-negotiate siyo haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wamekwenda mbali sasa hivi ni lazima watuhumiwa wafikishwe mahakamani, kama DPP anataka kufanya makubaliano na mtuhumiwa waende mahakamani, mahakama ijiridhishe kwamba makubaliano yale yanazingatia kwamba mtuhumiwa yule hajalazimishwa na hakuna mazingira ya mashinikizo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama tunataka kwenda suala ya plea bargain nimuombe Mheshimiwa Prof. Kabudi turudishe hapa hii sheria, isiwe wanajifungia chumbani mtuhumiwa na Mwendesha Mashtaka wa Serikali wanakubaliana wanakwenda kufanya plea bargain. Iwe ni kati ya mtuhumiwa, mahakama na DPP wakubaliane ionekane uwanja wa makubaliano ulikuwa sawa ndio mtuhumiwa aweze ku-bargain. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tena naomba nishauri twende mbali zaidi, twende tukafanye evaluation ya utekelezaji wa sheria ya plea bargain tangu tumeitekeleza. Wote hapa tuna smart phone mnaona twites za watu ambao wamefanya plea bargain, mambo ya kinyama yanayofanyika kwenye hizo magereza mpaka wale watu wanakubaliana kulipa zile fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, iundwe tume Maalum, kwa ajili ya kwenda kufanya uchunguzi na kupima ufanisi wa sheria hii. Watu wamenyanyaswa, watu wamenyang’anywa mali zao, wameporwa kupitia plea bargain, fedha zetu zimepotea hizo ambazo zimeshatolewa kwenye plea bargain, iundwe Tume Maalum kuangalia ufanisi wa sheria hii ambayo tumeitunga ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na twende mbali zaidi nimuombe Mheshimiwa Prof. Kabudi anapokuja kuhitimisha atueleze fedha zetu za plea bargain zimepoteaje! Attorney General akafanye uchunguzi kwanza zile pesa zilikuwa shilingi ngapi? Ambazo zilifanyika kwenye plea bargain. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, umenipunguzia muda wangu mpaka dakika tano na naheshimu Kiti chako. Naomba niende kumalizia hoja moja tu. Au umeniongeza mama! (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie hoja moja ya Katiba mpya; Mama amesema vizuri na amesema kwa kututia matumaini kwamba tusubiri kidogo, sisi wengine ni wasukuma kidogo hatuelewi maana yake ndio mpaka amalize au nini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kikubwa ninachotaka kusisitiza na kumuomba mama yetu suala la Katiba Mpya yeye alikuwa ni Makamu Mwenyekiti wa Bunge la Katiba. Anajua shauku ya Watanzania kwenye Katiba Mpya. Anajua gharama zilizotumika kuhakikisha Katiba imefikia ilipofikia na pengine ipo hatua za mwisho kabisa. Tunaheshimu kauli yake basi kidogo hii ya Mheshimiwa mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan angalau basi isitufikishe kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Kwa sababu hapo ndipo tunapoanzia kuchefuana, tusifike huko, ajitahidi kidogo hii iwe ndani ya hii miaka miwili akishakuwa Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi basi asimamie ilani yenu ya Chama Cha Mapinduzi. Nakushukuru sana. (Makofi/Kicheko)
Muswada wa Sheria ya Shirika la Mawasiliano Tanzania wa Mwaka 2017
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kipekee na mimi niweze kuchangia Muswada huu wa Shirika la Simu Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma kwa makini sana maelezo ya Mheshimiwa Waziri, Profesa Makame Mbarawa aliyoyatoa akiomba tupitishe Muswada wake wa kumpatia shirika hili na katika maelezo yake anasema moja kati ya madhumuni yake eti anataka kulipatia Shirika la Mawasiliano ya Simu jukumu la kusimamia miundombinu ya kimkakati ya mawasiliano nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, shirika hili lilianza shirika, ikaja kampuni sasa tunarudi kwenye shirika, lina miaka zaidi ya 40. Bahati nzuri ndugu yangu Profesa Makame Mbarawa amekuwa kwenye system hii ya mawasiliano kwa muda mrefu, alikuwa huko na mpaka sasa amekuwa Waziri. Juzi alikuja hapa wakatulisha ubwabwa, wakasema kwamba wanazindua TTCL, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuwepo kama mgeni rasmi, mpaka leo sijaona ushindani kati ya TTCL na makampuni mengine ya simu yaliyoko Tanzania. Sijauona ushindani wa aina yoyote ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaongea habari ya 3G, 4G, 2G peke yake line ya TTCL ukiiweka kwenye simu hizi ndogo ndogo za tochi haifanyi kazi. Line ya TTCL ukitoka three kilometers radius kutoka maeneo ya mjini au kwenye highway haishiki. Leo tunataka kumpatia Profesa na Wizara yake jukumu la kwenda kusimamia TTCL ambayo kimsingi ameshindwa kui-manage asimamie hiyo pamoja na makampuni mengine ambayo kimsingi kwake ni giants kwenye masuala ya mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda namna hii inabidi tuwe makini sana kwa sababu wakati mwingine inawezekana tunafanya hivi ili kujifurahisha lakini kweli leo tunarudi kwenye shirika kuipa ruzuku, kui-breast feed TTCL yenye miaka zaidi ya 40. Ina miaka zaidi ya 40 inataka breast feeding ili iweze kukua iende ikashindane na makampuni mengine maana tunasema sijui database na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inabidi Waheshimiwa Wabunge tulifikirie mara mbili suala la TTCL na suala la kwenda kwenye shirika la simu. Mimi ninachokiona hapa tunarudi kwenye ujamaa. Tunarudi kwenye Sera ya Ujamaa ya kutaka kwa vile TTCL yetu imeshindwa kushindana na makampuni mengine ya simu sasa tunataka kuyadhibiti ili angalau twende pamoja wakati tunazidi kuchelewa. (Makofi)

Mheshima Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge tujaribu kusajili line ya TTCL leo. Ukisajili line ya Tigo, Vodacom dakika tano unakuwa uko hewani, TTCL ukienda kusajili kwa wakala itakuchukua saa moja mpaka masaa mawili ili uweze kuwa hewani. Sasa mimi najiuliza Mheshimiwa Makame Mbarawa amekaa siku zote hizi, hebu kwanza atupe update tangu tumekula ubwabwa wa uzinduzi wa hili suala amefikia wapi? Au ndiyo leo anakuja na gear hii kesho unabadilisha unaingia na gear hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu Mheshimiwa Waziri atueleze amefikia wapi miaka miwili na nusu akiwa kama Waziri katika Sekta hii ya Mawasiliano kuhuisha kampuni ya Kitanzania ya mawasiliano kushindana na makampuni mengine na ndiyo maana unaona hata Wabunge wakisimama humu ndani leo hawaombi upeleke mnara wa TTCL wanasema leta Halotel, wanasema leta Voda, hamna mtu anataka habari ya TTCL.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama tumeshindwa kushindana kiuchumi kwa kufuata fair competition tusitumie mwanya kwa sababu sisi ni Serikali eti tuseme tunaenda kukandamiza private sector. Tusitumie mwanya huo kwa sababu mwisho wa siku tutakosa hata hao wawekezaji. Tunawakaribisha kwa mbwembwe na vigelegele na nini karibuni mazingira yako conducive, mwisho wa siku mbele ya safari tunaanza kubadilisha magoli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye Muswada huu wameweka mazingira ya kuwa-favour wao. Wanasema ili mtu aweze kuwa Mwenyekiti wa Bodi anatakiwa angalau awe na uzoefu wa miaka nane. Kama hiyo haitoshi kufanya kazi miaka mitano, hivi kweli, hawawezi kuiga mfano kwa wenzenu?

Mheshimiwa Naibu Spika, leo makampuni ya simu yaliyowekeza hapa Tanzania wanatumia wasanii tu kijitangaza na mambo yanakwenda, utasikia mara leo haliishi bundle, mara leo halichachi, mara nini, kampuni inasonga mbele, lakini sisi tulichokalia ni kutengeneza yale mazingira ya bureaucracy na urasimu mle ndani ili kusudi tu ionekane kwamba hii ni kampuni ya Serikali, kiukweli sioni sababu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Makame Mbarawa ampime mtu utendaji kazi wake kwa jinsi ambavyo alivyo creative, ampime kwa competency yake, ampime kwa jinsi gani anamletea matunda na siyo kukimbia mara anataka shirika, mara leo corporation, mwisho atasema iwe NGO. Tafadhali sana, tunamwomba awapime kwa competence. Leo mtu anayeweza kukaa kwenye Bodi akamletea mabadiliko akimchukua kwenye makampuni mengine ya simu hampati mtu wa miaka 56 au 57 anayemtaka yeye, hampati!

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo vijana wadogo wanafanya kazi, afungue boksi Mheshimiwa Waziri apate watu ambao watamsaidia kusukuma kazi siyo kila siku anacheza na makaratasi, anabadilisha sheria hii, anaweka urasimu huu, haitamsaidia wala haitaisaidia Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Simu (MTN) South Africa, leo mimi nikisikia habari ya MTN cha kwanza ninachokifikiria ni South Africa, wamei-brand ile kampuni ya simu ya nchi yao ili popote itakapokuwa inapita ionekane kwamba ni nchi yao. Tunao vijana wazuri wanaocheza mpira, wanaigiza sanaa wako kimataifa, yuko Mbwana Samatta, amtumie, anatumika kwenye matangazo mengine huko, atamsaidia hata bure kwenye Instagram yake ata-post TTCL. Kwa nini tusitumie marketing strategy na tuwe business oriented ku-push hii TTCL.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naiona a hidden agenda ya kurudisha hii mambo ya shirika, sijui corporate, sioni nia njema ya dhati ya Serikali kutaka kusukuma maendeleo. Tumesha-invest vya kutosha, tumeweka pesa nyingi kwenye mashirika ya umma lakini sijaona mafanikio makubwa kama nguvu inayoingia, sijayaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nataka nimuulize Mheshimiwa Makame Mbarawa hili suala la upigaji kura, aje atueleze hapa, tukija kupiga kura kwa sababu hili suala kwa mujibu wa Katiba, Ibara ya 98(b) ukisoma pamoja na Orodha ya Pili ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Nyongeza ya Kwanza inasema jambo la simu ni jambo la Muungano. Sasa Mheshimiwa Waziri aje atueleze hapa wakati tunapiga kura tutatafuta ile theluthi mbili ya Zanzibar na theluthi mbili ya Tanzania Bara au upigaji kura utakwendaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, natamani kufahamu kwa sababu ninavyofahamu Wazanzibari hawajanufaika kwa namna yoyote na uwepo wa kampuni hii ya simu. Leo tukisema tunarudi kwenye suala la shirika tunarudi kulekule ambako wanasema jiwe walilolikataa waashi, ndiyo tunarudi kulekule, sasa tuone kama kweli tukipiga kura watarudi kuchagua hili suala la shirika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuko kwenye dunia ya ubepari siyo dunia ya ujamaa kwamba leo tukiona tumezidiwa mchezo tunabadilisha magoli, hatuko huko. Tunahitaji kuona Kampuni ya Tanzania, mimi leo utaniita siyo mzalendo natumia makampuni mengine ya simu kwa sababu hivi kweli nitasikia raha gani niko mbali na familia yangu nikishika simu yangu kutwa inaniambia hakuna network? Nitasikia faraja ya namna gani? Natamani nikishika simu nasafiri kwenda kwangu Kahama kule Shinyanga mtandao uwepo, lakini leo TTCL mikoani haipatikani na zaidi ya yote ni simu ya watu ambao ni matajiri, wanaoweza kumiliki smart phone kwa sababu inashika 3G na 4G peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, of course inaleta assurance kwamba ukiwalazimisha Ofisi zote za Serikali na Idara zake watumie TTCL utapata wateja zaidi ya milioni saba au milioni nane, lakini hivi kweli wanaturudisha kule ukienda kukata leseni unaambiwa mtandao umebuma, wanataka waturudishe kule ukienda bandarini kulipia unaambiwa mtandao uko down. Huwezi kuwalazimisha watu watumie huduma mbovu unayoitoa eti kwa sababu wewe ni Serikali na wala hatuwezi kukubali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme leo Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atueleze tangu amepewa dhamana ya kuwa Waziri wa Mawasiliano amefanya nini kuhuisha TTCL ili iweze kutumika na kushindana na makampuni mengine ya simu Tanzania. Siyo tu hivyo, aje atueleze hapa nini mkakati wake atakapopewa huu uwakala wa kusimamia makampuni mengine ya simu ilhali tulishaingia kwenye mikataba tukakubaliana na wawekezaji waliokuja kuwekeza kwenye industry ya mawasiliano kwamba mchezo utakuwa fair. Nini strategy ya Serikali juu ya hilo?

Mheshimiwa Naibu Spika, kweli tunasema Tanzania ni kisiwa cha amani, ni eneo ambalo unaweza kuwekeza, lakini kwa mazingira ninayoyaona, tunawatisha wawekezaji kwamba Tanzania utawekeza leo, miaka mitatu au minne mbele hali lazima itabadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekaa nafikiria kuhusu suala la Data Centre kwamba iwe managed na TTCL. Mheshimiwa ananicheka, labda kama tunaliongea hili kisiasa lakini tukiliongea kibiashara kwamba tunatafuta biashara Tanzania TTCL ifanikiwe tupate hela halafu leo unasema lazima iwe managed na one centre source, mimi hainingii kichwani. Tushindane kwa hoja, tushindane kibiashara, tusitumie rungu la Serikali kwamba kwa sababu sisi ni Serikali tuna uwezo basi kila siku sisi tunaibuka na matamko, kila siku sisi tunaibuka na malekezo, mara tumebadilisha sheria, hapana. Tanzania ni nchi conducive for investment, hatuwezi kufikia hatua ya Mataifa mengine ambayo watu wanakimbia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wangu hii hoja aliyoleta Mheshimiwa Makame Mbarawa sijaielewa yaani naona anazidi kuturudisha ambako hata sisi hatukuwepo maana hiyo miaka hata sikuwepo, ndiyo anatupeleka huko. Tulisoma kwenye vitabu vya historia darasani ndiyo anaturudisha huko halafu tena anatuchanganya. Twende kibiashara, aendeshe TTCL kama kampuni ya kibiashara, watu wale wawe answerable. Huwezi kuniambia ili ufanye kazi kwenye kampuni ya simu, Joti amesomea mambo ya simu?

Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi ukaniambia ili ufanye kazi kwenye kampuni ya simu lazima uwe na uzoefu wa miaka nane, mimi hicho kitu sikubaliani nacho, Joti amesomea mambo ya simu? Wako vijana machachari tufanye marketing, advertisements, investment, tutumie resources tulizonazo tupambane na mashirika mengine duniani. Hata ukiweka Mlima Kilimanjaro kwenye TTCL watu watanunua line ya TTCL lakini usiniambie leo unaenda kushindana na watu kwa kuwaambia eti unataka kutengeneza mkakati, wewe mkakati wa kwako mwenyewe umeshindwa kuutengeneza, utaweza kutengeneza mkakati wa mashirika mengine? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata darasani anayechaguliwa kuwa monitor ni yule anayefaulu, huwezi kuwa monitor darasani wakati unafeli. Sisi tumeshafeli kwenye TTCL, sasa tumeona hapa tutafute ukiranja ili mwisho wa siku mtu akiongea unamwambia kaa chini, wakiibuka hawa kaa chini, kama ambavyo inafanyika kwenye mashirika mengine mengine sitaki kuyataja nitachangia siku ikifika. Tushindane kwa hoja, tushindane kibiashara, mambo ya kuleta usanii wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 2) wa Mwaka 2018
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba na marekebisho haya ya sheria mbalimbali za nchi yetu. Kwanza kabisa siku ya leo ikiwa ni siku maaalum nianze kwa kumtakia uponyaji mwema Mheshimiwa Tundu Lissu ambaye kimsingi yeye ni moja kati ya watu waliopelekea baadhi ya marekebisho makubwa ya sheria ya Chama cha Mawakili Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze pale alipoishia Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, suala la kutenganisha Chama cha Mawakili kwamba viongozi wa chama hicho wasiwe wanasiasa linakiuka Katiba kwa kiasi kikubwa na linakiuka Katiba kwa sababu siasa ni maisha na maisha ni siasa, huwezi kuvitenganisha leo humu Bungeni tunao viongozi wa vyama mbalimbali vya kitaaluma, wapo viongozi wa bodi ya mainjinia, wapo viongozi wa bodi ya wahandisina na viongozi wa Chama cha Mawakili pia wanayo haki ya kuwa Wabunge na wanaokuwa na haki ya kuwa wawakilishi katika taaluma yao. Hilo tunapaswa tuliangalie kwa makini kwa sababu mimi naliona linachukuliwa zaidi kwa kulenga baadhi ya watu fulani na sio sheria kama tulivyofundishwa utungaji wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda mbele zaidi naomba nijielekeze kwenye sheria marekebisho ya sheria inayohusiana na Administrator General wa RITA. Waziri ameleta marekebisho anasema Mkurugenzi..., wameandika kwa Kiswahili lile neno nalo ni gumu, lakini ni Administrator General na Deputy wateuliwe na Mheshimiwa Rais. Hawa watu ukisoma katika moja kati ya majukumu ya Administrator General au hiyo taasisi moja kati ya majukumu yake ni kusajili bodi za wadhamini, wanasajili bodi za wadhamini wa vyama vya siasa, mambo ya kidini na mambo ya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Mwenyekiti wa chama cha kisiasa. Unapompa mamlaka ya kumteuwa mtu anayesajili bodi ya wadhamini wa vyama vya kisiasa na mwenye mamlaka ya kufuta bodi hiyo ya wadhamini unaondoe ile impartibility condition ambayo administrator general anatakiwa kuwa nayo. Leo tunaweza kuona ni sawa kwa sababu Mheshimiwa Rais ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, lakini sisi watunga sheria lazima tujue leo kwako kesho kwangu, kesho itakapokuwa kwa upande mwingine Mwenyekiti wa chama kingine akapewa mamlaka ya kuteua Administrator General na Deputy wake madhara yake yatakuwa makubwa kwa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaiondoa ile dhana ya demokrasia ambao imejengwa na waasisi wa Taifa hili, mimi namshauri Mheshimiwa Waziri tuweke na sio tu kwa sababu ni Mwenyekiti wa chama lakini tuangalie mambo ya cheques and balance hebu angalia Mheshimiwa Rais akikosea kumchagua Administrator General, nani anaweza kutengua jambo hilo.

Nimesikitishwa na kufutwa mfano uliowekwa kwenye kitabu cha hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwa sababu umetolewa mfano ambao uko dhahiri. Sasa kwa sababu aliyevurunda kwenye kitu hicho yuko humu ndani amepata mamlaka ni ukurasa wa ngapi samahani naomba nisome, ukurasa wa tano imeelezwa vizuri tu Mheshimiwa Waziri wa Sera, Uratibu na Bunge aliwahi kufanya uteuzi wa Mkurugenzi Kukaimu nafasi ya Mkurugenzi Mtendaji wa NSSF na kwa sababu alikosea Rais alipata mamlaka ya kutengua uteuzi ule, lakini kwa sababu Waziri huyo yuko humu ndani amepata Mamlaka ya kufuta kwenye Hansard na sisi tunasema Alhamdullah. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapotaka kutoa mifano ambayo imetokea kwenye Taifa hili sio discussion power ya mtu mmoJa hili ni suala la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niseme hivi tunaposema ukimweka Administrator General ateuliwe na Mheshimiwa Rais tutakuwa tunakosa nafasi ya kurekebisha Administrator General kama a-fit kwenye ile position. Tunapomuweka Waziri awe na mamlaka yale endapo Waziri akikosea au Administrator General akishindwa ku-perform Mheshimiwa Rais an a fursa ya kumbadilisha yule Administrator General ndio mfano wangu na ndicho alichokikiri Mheshimiwa Jenista hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina nia mbaya tumeona teuzi nyingi zinafanyika kimakosa, tumeona wateule wengi wanashinda ku-perform to the expectation of the government tunawezaje kuwatoa wakiwa hawa watu ni Presidential Appointees. Wakati mwingine tujifunze kutokana na makosa kuhusiana na jambo hili ndio maana tunasema fursa inapotokea Waziri hafanyi vizuri au ameteua mtu aliyeshindwa ku-perform vizuri tunapata entrance ya kuweza kumuweka mtu atakaye-perfom kwa maslahi mapana ya Taifa hili kupitia kiti cha Rais and that is my all point. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niende moja kwa moja kwenye sheria najua hilo Mhsehimiwa Waziri amelichukua niende kwenye sheria ya urejeshwaji wa mali zitokanazo na uhalifu ambayo ni sehemu ya 13 ya marekebisho na ni Sura ya 256.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii samahani Mheshimiwa Waziri anasema Mkurugenzi wa Mashtaka kuweza kuwasilisha Mahakamani maombi ya upande mmoja yaani asikilizwe yeye peke yake, maombi ya kukamata mali iliyopatikana kwa njia ya uhalifu ambayo ama iko hatarini kupotea au kuharibiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukishuhudia kwenye Taifa hili watu wanakamatiwa mali zao, wakati mwingine ni kwa hila tu wala hakuna uhalali wowote wa kukamata zile mali, watu wanafungiwa akaunti zao kwa hila tu basi hilo tuliache. Lakini kesi inaendelea Mahakamani mali zinakamatwa mtu anashindwa kuendesha maisha yake, anashindwa kuendesha biashara hilo tumeliacha leo huyo Mwendesha Mashtaka kabla Mahakama haijaamua kama zile mali ni za uhal ifu ama sio za uhalifu anapeleka maombi mali zile ziuzwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatengeneza mazingira hapa ya kutaka kuwafanya watu wawe wanyonge ndani ya Taifa lao. Nafasi hii ni rahisi sana kuwa kutumika vibaya na Mwendesha Mashtaka na hii ni kama tu msingi wa ile hoja ya hati anayopeleka Mwendesha Mashtaka ambayo umefutwa kimahama anapeleka kuzuia mtu asipate dhamana kwa sababu yaani sababu anazozijua yeye mwenyewe na haulizwi mahali popote, ile ilifutwa kwa msingi kama huu kwa sababu Mwendesha Mashtaka anaweza kum- misuse powers alizopewa. Mimi niiombe Serikali kwanza maombi ya kuweza kuziuza mali zile yasiwe exparte, yasikilizwe kwa pande zote mbili. (Makofi)

Mheshimiwe MWenyekiti, lakini pili maombi yale iwe ni desecration ya mahakama ku-decide kwamba mali zile ziweze kuuzwa ama zisiuzwe bila kumathiri mmiiki wa malizile kwa sababu kwa nchi hii ya leo unapokwenda najisikia vibaya kusema hivi kumekuwa na uvunjwaji mkubwa wa kanuni, sheria na taratibu hasa kwa Serikali ambayo tunaambiwa kila mtu ambaye ameteuliwa na Serikali hamna neutral, lazima kwanza mezani ukae na Ilani ya Chama cha Mapinduzi na hakuna neutral lazima uegemee upande wa Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali tuliyofikia sasa hivi uhuru wa Mahakama hawa Mawakili huko hali ni mbaya wote wameambiwa wanatekeleze ilani ya Chama cha Mapinduzi, kwa hali hii tukaruhusu na mali za watu zitaifishwe na kuuzwa, watu watafilisika, mali imeshauzwa, Serikali yenyewe hii iko hoi bin taabani ikija kuonekana mtu yule mali zake ni halali atachukua miaka 100 kuja kulipwa mali zake na kuirudishiwa.

Kwa hiyo, mimi niombe ombi kwa Mheshimiwa Waziri tuondoe suala la exparte kwenye maombi ya kuuza hizi mali, lakini iwe ni desecrationya Mahakama, uhuru wa Mahakama uzingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwe Mwenyekiti, mwisho kabisa niongelee hili suala la ushahidi wa ku-record kweli ni mzuri, mnasema kwamba shahidi atarekodiwa ushahidi wake na atapewa nakala. Niombe tunarudi kule kule sasa hivi tumekuwa kama watu ambao tunaishi kwa tahadhari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtuhumiwa anahojiwa yuko mahabusu, anamaliza kuhojiwa kwa video na picha anaambiwa anapewa nakala yake anaipeleka wapi? Uwezekano ni mkubwa sana kwa Waendeshwa Mashtaka
ku-temper na hizi document kwa hali ilivyo. Mimi nawapenda sana Waendeshwa Mashtaka na ni taaluma yangu lakini niseme tumefika pabaya lazima tupige ndulu. Ushahidi huu uandikwe kwa maandishi, usainiwe na chini ya yule anayechukuliwa ushahidi huu uwe chini ya mwanasheria, uwe chini ya wakili, usainiwe ndipo akabidhiwe ili...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Nakushukuru sana kwa interest ya muda nakushukuru sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa wa Mwaka 2018
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nitoe mchango wangu kwenye sheria hii muhimu kwa Taifa letu inayohusu vyama vya siasa.

Mheshimiwa Spika, mimi nianze kwa kulitaarifu Bunge hili kwamba Ibara ya 20(1) ya Katiba inatoa uhuru wa kuunda vyama vya siasa na Ibara ndogo ya (2) inaeleza mambo ambayo yanapaswa kuzingatia katika uundwaji wa vyama vya siasa na ukiyakiuka mambo haya basi chama hicho kinaweza kikafutiwa usajili. Vilevile ibara ya 3 inasema Bunge linaweza kutunga sheria inayoweka masharti yatakayohakikisha kwamba vyama vya siasa vinazingatia mipaka na vigezo vilivyowekwa katika Ibara ya 2 hapo juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Katiba hii hakuna hata sehemu moja inayoonesha kwamba Msajili anaweza kumfukuza mtu kufanya kazi za siasa kwa sababu amemkosea, haipo hata sehemu moja, lakini muswada ulioletwa na Msajili wa Vyama vya Siasa unampa nafasi hiyo Msajili kinyume kabisa na Katiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikufahamishe kwamba jambo hili halijaja kwa bahati mbaya, tunamfahamu sote hapa Jaji Mutungi, Mheshimiwa Waziri Jenista, Attorney General na tunaifahamu Serikali vizuri hawa ni watu ambao wangeweza kukaa chini na kuleta muswada ambao unakwenda sawa na matakwa ya Katiba, lakini wamefanya hivi kwa makusudi kwa sababu Kanuni za Bunge zinataka, kwamba mapendekezo ya kamati yanayokwenda kwa Serikali yarudishwe kwenye kamati wapitie kama kweli wametimiza yale ambayo Serikali imekubaliana na Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumepata majibu ya mapendekezo ya Serikali leo asubuhi hapa Bungeni na kwa kukufahamisha tu kwenye mapendekezo ya Serikali yaliyoletwa yapo mambo mengi ambayo tuliafikiana kwenye Kamati hayajafanyiwa marekebisho. La yamefanyiwa marekebisho sivyo Wajumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria walivyopendekeza.

Mheshimiwa Spika, haya mambo hayafanyiki kwa bahati mbaya… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Salome kidogo dakika mbili tu, utaendelea. Mheshimiwa Mchengerwa wewe ni Mwenyekiti wa Kamati.

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Spika, ndiyo…

SPIKA: Yuko wapi Mheshimiwa Mchengerwa?

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Spika, nipo.

SPIKA: Haya maneno yanayosemwa ikoje maana yake tulikubaliana kwamba mtapitia kabla.

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Spika, Salome Makamba sio Mjumbe wa Kamati yangu kwa hiyo hana ufahamu wa yale ambayo yamerekebishwa na jedwali la Serikali. (Makofi)

SPIKA: Nakushukuru sana, sasa nimeelewa, kumbe Salome unaongea mambo ambayo… Salome endelea sikuwa na nia ya kumkata.

MBUNGE FULANI: (Alizungumza bila kutumia kipaza sauti)

SPIKA: No! no! no! Mimi nilitaka Salome tu nielewe maana yake alikuwa anasema kwamba hakushirikishwa ndio maana nikamnyanyua Mwenyekiti katikati ya mjadala, endelea Salome.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni za Bunge mimi kama Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ninayo haki ya kuingia Kamati yoyote na kwenda kushuhudia mwenendo wa Kamati na ikibidi naweza kutoa mapendekezo, kanuni inanikataza mimi kupiga kura tu. Kama Kanuni hii iko kwa bahati mbaya mimi naridhia na sitokwenda kwenye Kamati yoyote… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa yaani mimi ninachoona kabisa hujajiandaa. (Makofi)

Eh kabisa kabisa kwa sababu hakuna cha kuficha, ninamuuliza huyu Mwenyekiti nimekukata makusudi nimuulize kwa sababu niliagiza kwamba hii nanii ya Serikali ikishamalizika muione kabla hatujaenda Bungeni na amethibitisha. Sasa wewe ambaye hukuwa Mjumbe hebu iache ajenda hiyo maana yake unapotosha, eeh. Hiyo ajenda yaani iache tu, wenye Kamati yao wapo sio vizuri sana kupotosha mambo ambayo; wewe sema unataka kusema nini Salome?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haimruhusu Msajili wa Vyama vya Siasa kumzuia mtu kutengeneza chama cha siasa eti kwa sababu wazazi wake wote wawili si Watanzania, hairuhusu. Hayo ni masharti yalipo kwenye muswada mpya unaokuja na haya ni marekebisho baada ya mara kwanza kuwekwa sharti kwamba mtu haruhusiwi kutengeneza chama cha siasa ikiwa yeye mwenyewe si raia wa Tanzania kwa kuzaliwa. Yamefanyika marekebisho sasa wameleta aina nyingine wanasema ni lazima wazazi wako wote wawili wawe raia wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, mimi siamui nani anizae hapa duniani, kuzaliwa na wazazi wote Watanzania sio discretion power niliyonayo, ninajikuta nimezaliwa na wazazi mmoja si Mtanzania na mwingine ni Mtanzania. Hiki kifungu hakikubaliki; kwanza ni kinyume na Katiba, lakini pili Msajili hana hayo mamlaka ya kumuamulia mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbaya zaidi katika section 26(2) ya muswada huu Msajili amevikwa mamlaka makubwa zaidi ya kufuta chama.

Mheshimiwa Spika, leo kwako, kesho kwangu, lakini nakuhakikishia dua la kuku halimpati mwewe, hii sheria leo tunaitunga kwa kuangalia kesi zilizopo mahakamani za CUF, leo tunaangalia kwa sababu CHADEMA ni chama cha upinzani, lakini ninakuhakikishia wanasema hii sheria itakuja kuwachinja walioitunga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sidhani kama ni sahihi Bunge lako tulipotoshe kwa kumpa mamlaka makubwa namna hii Msajili wa Vyama vya Siasa kwa kudhani kwamba tunakomesha upande mmoja.

Mheshimiwa Spika, Msajili wa Vyama vya Siasa kazi yake kubwa na namba moja ni kulea vyama vya siasa. Ukiangalia sheria hii mpya iliyokuja kwako vifungu vingi vinafanya kazi ya kubadilisha kazi ya siasa kuwa ni kazi ya jinai. Kosa dogo humu mtu anaweza akajishtukia amefungwa jela miaka mitatu mpaka miaka 20, kwa kosa dogo tu. Sheria hii inakwenda kupita kimya namna hii tunaruhusu, kazi ya siasa ni kazi ya kujitolea, hakuna watu wanaolipwa kwa ajili ya kufanya kazi ya siasa, lakini tunaruhusu mtu afungwe jela kwa kosa dogo miaka mitatu mpaka karibu miaka 20 na faini juu au vyote kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika,…

SPIKA: Si ungekuwa unatoa mifano Salome ili watu wakuelewe unasema kwa kosa fulani…

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Nimesema section 26(2) isomwe pamoja na Ibara ya 8(c) na (e) ya marekebisho na section zingine zinazofanana na hizo, zipo nyingi sana. kwa ajili ya interest ya muda naomba nitaje hizo chache.

Mheshimiwa Spika, tulisema wazi kwamba ili kuepuka mgogoro kama uliojitokeza kwenye kikokotoo, namna ya kutengeneza coalition terms and conditions zielezwe kwenye sheria moja kwa moja na sio kwenye kanuni, tunalieleza hilo. Katika eneo la coalition nyuma tumeweka schedule tumeonesha namna gani muungano wa vyama vya siasa unaweza kuundwa, lakini katika sheria hii minister anakwenda kutafsiri yale yaliyoandikwa kwenye sheria mama juu ya muungano wa vyama vya siasa. Tunayo sababu ya kuliangalia hilo kwa kina kabla hatujafunga muswada huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kwenda haraka niende kwenye suala la kufuta vikundi vya ulinzi. Mawakili na wanasheria wenzangu wamepotosha suala lililoandikwa kwenye Katiba la uundwaji wa majeshi. Vipo vikundi mbalimbali vya binafsi vya ulinzi tena vinakwenda mbali zaidi wanapewa rank za kijeshi, wanabeba silaha na wanapewa mafunzo ya kijeshi. Vikundi vya ulinzi tunavyoviongelea hapa ni vile vya mtu kujilinda mwenyewe au wanachama kulinda mali zao cha chama.

Mheshimiwa Spika, leo tunasema hao wamekatazwa na katiba, katiba haijakataza Wabunge wenzangu kwenye hili lazima tusome kwa makini kwa sababu tutapotoshana, haijaelezwa hivyo. Tunao KK Security na Ultimate Security hivyo ni vikundi vya ulinzi na vipo kwa mujibu wa sheria na Katiba. Kwa hiyo, sitaki kuamini kama vikundi vya ulinzi leo eti ni kosa kuwa navyo kisheria mpaka Msajili wa Vyama vya Siasa anataka kuvifuta.

Mheshimiwa Spika, ninachokiona hapa tunalo ombwe kubwa sana juu ya Serikali yetu upande wa Jeshi la Polisi kuwalinda raia. Sijawahi kumuona Katibu Mkuu wa CHADEMA Ndugu Vincent Mashinji anaongozwa na kimulimuli cha polisi wala kulindwa na polisi, tunamlinda wenyewe Katibu Mkuu wetu, lakini juzi Mizengo Pinda amefanya maandamano jambo ambalo limezuiliwa, amesindikizwa na polisi. Bashiru akizunguka mikoani anasindikizwa na polisi… (Makofi)

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, Kuhusu Utaratibu.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Sijawahi kuona hata siku moja viongozi wa Chama cha CHADEMA au chama chochote cha upinzani wanasindikizwa na polisi…

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, Kuhusu Utaratibu.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, Waziri Mkuu wawili wa wastaafu wapo CHADEMA…

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, Kuhusu utaratibu.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wako wa Kamati ya Kanuni, mtu anaposimama anataka kutoa utaratibu anatakiwa ataje kwanza kanuni gani, wewe ndiye umenifundisha hayo, mimi naachana nayo.

Mheshimiwa Spika, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) tunao Mawaziri Wakuu wawili wastaafu, lakini wanatembea/wanafanya ziara kwenye Taifa hili hakuna hata mmoja amewahi kwenda na hicho kimulimuli. Kwa hiyo, kabla hatujaenda kwenye suala la kupitisha kwamba polisi ndio watulinde nafikiri tuanze kujadili impartibility ya Police Department kwenye taifa hili. Nafikiri huo ni mjada mpana ambao ni lazima tuujalidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.5) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi nichangie kwenye Marekebisho haya ya Sheria, Marekebisho Na. 5 ya mwaka 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa utangulizi kwamba ukisoma Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 64 jukumu la msingi na kubwa la Bunge letu Tukufu ni kutunga Sheria na kwa umuhimu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kushauri kwamba tutenge muda wa kutosha katika mchakato wa kutunga na kufanya marekebisho ya sheria na ninayasema hayo kutokana na msingi wa namna ambavyo Bunge letu linaendeshwa muda tunaowapa Wadau kuwasikiliza ambao hao ndio walaji wa Sheria tunazozitunga ni mchache sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe tu Serikali na niombe Bunge letu Tukufu tuitumie vizuri fursa hii tuliyopewa ya Kutunga Sheria kwa kuwasikiliza wananchi na hii itafanya Tutunge Sheria ambazo zinatekelezeka na nita cement hoja yangu hiyo kwa kuanza na Sheria hii ya Sheria ya Mawasiliano ya Kielektoniki na Posta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko Na. 10 yanasema yanalenga kumpa adhabu mtu anayetumia, simu card ambayo haijasajiliwa. Nimefikiria sana ni kwa mazingira gani kwa sababu Serikali wakati inatuambia tusajili line zetu za simu humu ndani walituhakikishia kwamba kwa kufanya hivyo watadhibiti wale wote ambao wanatumia line za simu vibaya na picha waliyotuonyesha humu ndani ni kwamba kwa kudhibiti huko haitawezekana kwa namna yoyote mtu kumiliki kadi ya simu kama hajasajiliwa. Sasa swali ambalo nataka nimuulize mtoa hoja leo, ni mazingira gani hayo anayotaka kutueleza baada kweli ya huu mfumo wa kusajili line za simu kufanikiwa ni mazingira gani hayo ambayo mtu atatumia line ya simu bila kusajiliwa na Kampuni inayomiliki sim card isiwe na taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watujengee hayo mazingira ili tusaidie kuwashauri, nadhani kifungu cha juu kabla ya kifungu hiki cha kumwadhibu mwananchi anayetumia line ya simu bila kusajiliwa Kifungu kilichotakiwa kutangulia ni kuiadhibu Kampuni ya line ile ya simu kwa kumruhusu mtu yule ama kwa kujua au kwa kutokujua kutumia line ya simu ambayo haijasajiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri tuanzie hapo, tofauti na hapo mimi Napata nia ovu ya Serikali ya kutaka kugeuza suala hili la kutumia line za simu bila kujua kama mwanzo, yaani moja ya chanzo cha mapato cha Serikali kwa sababu sioni mantiki yoyote ya mtu kutumia line ya simu bila kusajiliwa. Namna pekee ambayo nimeweza kuifikiria tangu nimeanza kusoma Muswada huu ni pale ambapo nitakuwa na line ya simu ambayo ni ya Mataifa mengine, lakini bado line hiyo imesajiliwa kwenye Mataifa hayo. Kwa hiyo, niseme tuanze kwanza kuiadhibu Kampuni kama ni Vodacom, Airtel, Tigo mtu anaposhikwa na line ya simu baada ya huo muda ambao tumejiwekea wa kufanya registration ishikwe yenyewe ieleze ni kwa mazingira gani, kwa sababu haya ni mambo ya kielektroniki, hayana, hayana bla blaa!

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa namna gani mtu ameweza kutumia service yao bila wao kupata taarifa, baada ya kusema hayo nataka nihamie kwenye Sheria ya BASATA marekebisho yaliyoletwa na Waziri wa Michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya nchi hii ya sanaa na michezo na lengo la uanzishwaji wa BASATA ilikuwa ni kulea wasanii, na kulea ni kuwawezesha Wasanii, kwanza tuwe na wasanii wengi, lakini uwawezeshe wasanii wale waweze kufanya vizuri, Kitaifa na Kimataifa, na wanapokosea uwaite wasanii na kuwaonyesha njia sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa faida ya wengi nataka nisome Kifungu cha 18 cha Marekebisho haya halafu tuone kama kweli, kweli hii ndiyo nia dhahiri ya BASATA, okay, Kifungu cha 18(2) kimeandikwa kwa kiingereza na kinasema “The Council shall have the power in it is capacity as a body cooperate for the purpose of caring out it is functions to rate, kazi ya kwanza hiyo ya Baraza, ni ku-rate, to Inspect, wanafanya Inpsection to arrest, pamoja na mabadiliko ya Serikali wanasema wamefuta arrest wanaweka ku-seize, wanaweza ku-seize to suspend or destroy any work of art being produced displayed nakadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ambayo ita –contravene na hii Sheria, hawa jamaa wanajipa nguvu mpaka ya kukamata, mpaka ya ku-destroy, mpaka ya ku-seize. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawajui huyo msanii amehangaika kiasi gani kurekodi huo wimbo, hawajui huyo msanii amehangaika kiasi gani kuchonga hicho kinyago, hawajui huyo mlimbwende amehangaika kiasi as long as ana –contravene wata-destroy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijawahi kuona mzazi wa namna hii, sijawahi kuona, lengo lao sasa hivi imekuwa ni kucha, wanaenda mbali zaidi Kifungu gani hichi, kinaongelea habari ya faini, yes, ya mtu ambaye hajasajiliwa, wanasema artistic work, Kifungu Na. 10 nafikiri Artistic work ambayo mtu atafanya bila kusajiliwa watamtoza faini mpaka shilingi milioni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sanaa inahusisha kutengeneza Vyungu, sanaa inahusisha hawa watu wanao cheza maigizo barabarani, unaenda kumtoza shilingi milioni moja, pamoja na mabadiliko, walianza na milioni tano wakaja milioni moja, ndiyo maana nimeanza kusisitiza ni lazima tuwashirikishe Wadau, hawa Wadau wangekuja tusingesema habari za milioni moja na milioni tano, tungewasikiliza wangesema kutokana na uwezo wao. lakini hizi artistic work wanazosema zisajiliwe ni za namna gani, kwa sababu mwisho wa siku sisi tunatunga Sheria, na Sheria lazima iwe specific, haiwezi kuwa vague inasema any Artstic work, hii inajumuisha na yale maigizo ya shuleni, watoto wanaoimba kwenye graduation. Inajumuisha na wale wanaoimba kwaya Kanisani, maana ile nayo ni sanaa, na wenyewe hao ni lazima wasajili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mtoa hoja ni Mwanasheria alete Sheria ambayo iko specific inalenga watu specific najua lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba hawa watu wanatambulika ili waweze kulipa Kodi na waweze kunufaika na sanaa yao, kwa sababu hiyo Sheria ijielekeze kwa watu wa namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka haraka, niende kwenye Sheria ya Vitalu, hii Sheria inaitwa, inaitwa Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori, no, sorry, narejea kidogo, ahha, section. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Hujakariri.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, page 27 inaongelea habari ya Sheria ya Wanyamapori, ambapo Kifungu cha 54(11) kinasema “The Minister may in allocating hunting blocks use auction, tendering, or any other modality or system of allocation.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, what is that any other modality? Hizo ndiyo upenyo tunasema wa kumruhusu Waziri kufanya matumizi mabaya ya madaraka yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wanaifahamu hiyo njia nyingine yoyote ya kufanya minada tofauti na waliosema kwenye Sheria hii waiseme specific Bunge hili lifahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusitengeneze mianya ambayo huenda Waziri wa leo akawa na busara na hekima kubwa akaja kukalia kiti hicho Waziri mwingine ambaye hana busara akaamua tu kuamua any other method tofauti na zile ambazo zimesemwa kwenye Sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hichi Kifungu sikubaliani nacho naomba waweke, kama wanayo hiyo any other method waiandike specific kwenye Sheria au hiyo any other method ifutwe kwenye Sheria yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Muda.

MWENYEKITI: Malizia. (Kicheko)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihitimishe kwa Sheria hii ya Baraza la Mitihani, Sheria hii ni ya muhimu sana, na Wadau ni lazima washirikishwe, wametoka kusema wenzangu vizuri sana, kama tunataka kudhibiti Mitihani isiibiwe, kama tunataka kudhibiti watoto wasipewe mitihani, turudi pale pale tuwe specific tukisema mtu yeyote hatakiwi kuwa na mtihani unaongelea mtihani ule ambao ndiyo wanafanya kwa wakati ule au unaongelea any past paper ambayo imefanyika, kwa sababu past paper immediately baada ya kumaliza mtihani tayari hiyo inaitwa past paper.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukimkuta nayo baada ya mtihani, hiyo inakuwa ni sehemu ya ile kwenye hiyo Sheria, si sehemu ya mtihani ambao unasemwa hapa au mtihani ambao tayari umeshafanyika. Kwa hiyo, hili nalo pia limshauri Mheshimiwa Waziri ajaribu kurekebisha Kifungu hiki ili kiweze ku-reflect lile analotaka kulifanya, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa dakika hizi tano ningependa kuongelea mambo makubwa mawili. Jambo la kwanza ni ushiriki wa Watanzania kwenye ajira zinazohusiana na migodi na madini na jambo la pili, ukiacha ajira ni ushiriki wako katika manunuzi na uuzaji wa bidhaa kwenye migodi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao Watanzania wengi, tasnia ya madini imeanza kushamiri kuanzia miaka ya mwaka 1999/ 2000 wako Watanzania wengi wamehudumu kwenye sekta ya madini lakini hawatambuliki au hawajulikani wapo wapi. Ni mmoja wa wadau ambao tumefanya kazi kwenye sekta ya madini, nilikuwa naiomba sana Serikali itengeneze Kanzidata inayoeleweka itawatambua watumishi waliofanyakazi kwenye Sekta ya Madini. Na hii itasaidia kupunguza idadi ya watu wanaojiita ma-expert au wazungu ambao wanakuja kufanya kazi ambazo Watanzania wanaweza kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tumeshudia Watanzania wachache wanapata nafasi za juu Serikalini I mean sio Serikalini. Wanapata nafasi za juu kwenye migodi kwasababu Watanzania wale wamehudumu kwa muda mrefu. Tofauti na maeneo mengine ukihudumu kwa muda mrefu kwenye sekta za madini uwezo wako unakuwa ni mkubwa kiasi kwamba una uwezo wa kufanyakazi ndani ya Tanzania, ndani ya Afrika hata Duniani kwa ujumla. Kwasababu eneo hili utaalam wake hauna tofauti kwenye maeneo mengine ambayo kuna migodi mikubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimuombe sana waziri na hili ni tatizo la muda mrefu tumekuwa tunalipigia kelele kwa zaidi ya miaka sita, miaka sana, miaka nane hakuna Kanzidata ya pamoja inayowatambua wataalam hawa waliofanya kazi muda mrefu. Lakini sio tu Kanzidata, iwafuatilie haki zao watu ambao wanasifa za kufanya kazi kwenye managerial position katika migodi kwasababu wakati mwingine wanaondolewa kwa hila.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano; migodi ina system inaitwa blacklisting ukifanya kosa kidogo wanakuweka kwenye kitabu cheusi hutafanyakazi sehemu yoyote ile duniani. Vigezo vya blacklisting vinatokana na wale ambao wanakuja na hiyo migodi, mtu amekutwa na sigara kwenye mfuko wake wa suruali unakuwa blacklisted, umesomeshwa kwa gharama kubwa, wewe ni geologist, wewe ni operator huwezi kuajiriwa mahali popote. Tunataka Mheshimiwa Waziri uwalinde Watanzania; kwa kuhakikisha vigezo vya blacklisting vina-qualify na mazingira na utamaduni wa Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Watanzania wanaoweza kutoa huduma na bidhaa kwenye migodi yetu hasa wawekezaji. Wapo Watanzania wengi wenye uwezo, wenye fedha tena hata zaidi ya wale ambao wana supply kwenye migodi.

Mheshimiwa Spika, Tanzania tunazalisha bidhaa nyingi, tuki-customize, tukishusha chini viwango vya bidhaa zinazotakiwa kuwa supplied hasa vyakula, wakati mwingine apples zinapatikana Muheza Tanga lakini yule supplier anazitoa South Africa, hakuna sababu! Wamekuja Tanzania, you are in Rome, act like Romans. Wamekuja Tanzania watakuwa ma-apple ya Kitanzania na Watanzania wapo ambao wanaweza ku-supply kwenye migodi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri ili kulinda maslahi ya watu hawa ambao wanaweza ku-supply, best practice tulifanya wakati nahudumu kwenye Mgodi wa Buzwagi na hasa kwenye hili suala wanaloliita CSR na mambo ya local content. Kule mkienda kuwatafuta katika level ya ward (kata), mkaingia kwenye level ya wilaya, mkapanda mkoa mpaka taifa, dhana ya local content itatekelezwa vizuri lakini tukisema tu-generalize useme leo mchicha uchukuliwe Tanzania nzima au ukachukuliwe Dar es Salaam ni lazima utawaacha wazawa wa Shinyanga kwa sababu uwezo wa kuzalisha hauwezi kuwa sawa na wa maeneo mengine. Kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri kusimamia dhana hii ya local content tuwawezeshe na tuwape fursa Watanzania wanaoweza ku-supply kwenye migodi yetu.

T A A R I F A

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge anaendelea kuchangia kwamba siyo tu Watanzania wana uwezo wa kupeleka apples na vitu vingine, lakini wapo Watanzania wana uwezo wa ku-supply chemicals na vifaa vikubwa kwenye migodi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe Mheshimiwa achukue taarifa hii kwamba Watanzania wapo wengi wenye uwezo thabiti na wanakidhi mahitaji ya kuweza kufanya supply na kukidhi masharti yote kwenye migodi hii mikubwa. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Taarifa hiyo Salome.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa ya Mheshimiwa Saashisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemaliza dhana ya local content, nije kwenye suala la CSR. Migodi mingi wawekezaji wakubwa wakitupa hizi pesa za CSR wanadhani ni hisani; wanazileta pesa hizi halafu wanatupangia namna ya kuzitumia. Tunazo Halmashauri zetu kuanzia level ya kijiji, kata mpaka manispaa, tunavyo vipaumbele ambavyo vimepangwa na wataalam na wananchi, kama wanatupa pesa za CSR, wapeleke kwenye Baraza la Madiwani.

Mheshimiwa Spika, Baraza la Madiwani wanavyo vipaumbele, wala hawana haja ya kuchakata kwa sababu mwisho wa siku wasije wakatushauri tutengeneze bwawa la samaki Shinyanga Mwendakulima au Ibadakuli wakati pale asili yake ni semi desert. Kwa hiyo, walete kwenye level ya halmashauri, kule wana vipaumbele vyao, sisi tutatekeleza, tukishakamilisha mradi wenyewe wafanye shughuli ya kufanya malipo na kusimamia viwango vya ubora. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma, taarifa.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Napenda kumpa taarifa mjomba wangu Salome, nilikuwa nimeacha kumsalimia kwa sababu dishi liliyumba lakini leo mjomba wangu marahaba.

SPIKA: Lakini ninyi mnaopelekewa hizo hela za CSR, Mheshimiwa Musukuma wewe mweyewe umelalamika leo asubuhi zikija kule supervision peke yake wanakula milioni 600, mwingine amelalamika milioni 200, kwa hiyo maana yake zinakuwa squandered. Kwa hiyo, kupeleka huko halmashauri peke yake bado sio dawa.

Mheshimiwa Salome Makamba, dakika zako zilishaisha.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nimalizie. Umeongea vizuri sana na hoja yangu nilikuwa nataka nii-cement kwa kusema wasipewe pesa, waende wakachukue miradi ya vipaumbele kwenye halmashauri. Ikishatekelezwa kama ni ujenzi wa barabara certificate itoke, mgodi upelekewe certificate ufanye malipo. Wasipewe pesa zikaingizwa mle kwa sababu kuna risk ya re-allocation, mis-use, corruption na risk zingine. Wasipewe cash money isipokuwa watekeleze miradi ya vipaumbele kama ilivyofanyika kwenye D and OD kama ilivyotekelezwa kuanzia ngazo ya vijiji. Malipo yafanywe na mgodi siyo mgodi ndiyo unapanga halafu shule ya milioni 20 unajenga kwa milioni 50 wanakuja baadaye kusema wametekeleza CSR, CSR sio hisani ni haki ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie katika Bajeti ya Wizara ya Madini. Kabla sijaanza mchango wangu nataka nimsaidie tu kaka yangu Iddi, Mbunge wa Msalala kwamba kifungu cha 105 cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2019 kinaelekeza CSR utekelezaji wake ni lazima mipango yote ipangwe na halmashauri ikishirikiana na mgodi na halmashauri ni lazima itengeneze guideline ya namna ya kutekeleza CSR na imeweka haki zote za Baraza la Madiwani na Halmashauri kutekeleza. Kwa hiyo kama hawafanyi hivyo ina maana wametoa hisani kama watu wengine na hisani hiyo ni lazima itozwe kodi kwa sababu hawajafuata utaratibu wa kisheria.

Mheshimiwa Spika, tarehe 22/04/2020 nilisimama ndani ya Bunge hili Tukufu, pamoja na kashikashi zote nilisimama kwa ajili ya kuwatetea wachimbaji wadogo wadogo ambao wakiwa wanachimba sehemu kubwa ya mapato yao ilikuwa inachukuliwa na mtu anayeitwa mwenye shamba na fedha nyingine anachukua mtu ambaye anaitwa msimamizi. Leo kwa kweli kwa mara kwanza niseme tu nimpongeze Mheshimiwa Waziri alisilikiza kilio change, ametekeleza na sasa hivi kwa mara ya kwanza mchimbaji mdogo anapochimba na kupata dhahabu asilimia 70 ya mapato inakuwa ya kwake, huyo anayeitwa mwenye shamba anapata asilimia 15 na huyo anayeitwa msimamizi anapata asilimia 15. Mimi najivunia kwa sababu hoja niliyoisimamia imetekelezwa kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuchukua maombi yangu ambayo niliyasema ndani ya Bunge hili mimi nina mambo mawili ambayo nataka nimwombe Mheshimiwa Waziri ayasimamie. La kwanza, inaonekana kwamba asilimia kubwa ya watu ambao wana leseni za uchimbaji hawachimbi, wamezikalia leseni hizo. Hayo siyo maneno yangu, ripoti ya CAG inasema asilimia 58.3 ya watu wenye leseni za uchimbaji hawafanyi shughuli za uchimbaji, yaani ni leseni mfu.

Mheshimiwa Spika, vile vile ripoti hiyo inasema katika hiyo asilimia chache ambayo ya watu wanaochimba, asilimia 97 zaidi ya robotatu ya watu wanaochimba ni wachimbaji wadogo wadogo. Mheshimiwa Waziri naomba awanyang’anye leseni watu ambao wamezikalia leseni hizo na maeneo ya uchimbaji, hawafanyi shughuli za uchimbaji, badala yake wanawanyima fursa wachimbaji wadogo ambao wapo tayari kufanya shughuli za uchimbaji na wanajikuta wachimbaji wale wanachimba kwenye maeneo ambayo hayana potential ya kupata mali. Hilo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu la pili kwa Wizara hii; TRA wanakwenda kwenye masoko ambayo wachimbaji hawa wanakwenda kuuza dhahabu, masoko ambayo yameanzishwa hivi karibuni. Wakifika pale wanamkuta mchimbaji anauza dhahabu yake, tuseme milioni 200 au milioni 300, Waheshimiwa msishangae milioni 200 au 300 kwa mchimbaji ni hela ndogo sana akiipata. Anakwenda mtu wa TRA pale anamtoza ushuru kwa ile milioni 300 pato ghafi ambalo mchimbaji yule amelipata bila kujali kwamba kuna gharama za uchimbaji, bila kujali mtu yule amepata hasara kiasi gani, bila kujali kwamba mtu yule amewekeza kiasi gani? Sasa hawa wachimbaji wadogo mtu anaweza akachimba hata miaka 10 hajakutana na mali, anazika mtaji ardhini zaidi ya mamilioni ya fedha. Anapopata bahati anakwenda kuuza dhahabu yake anategemea angalau aweze, kuna watu wapo kwenye machimbo kule wana miaka zaidi ya 10 hawajawahi kuonana na familia zao.

Mheshimiwa Spika, naomba nimwombe Mheshimiwa Waziri akae pamoja na watu wa madini, wasitafute cheap income, hawa watu wana struggle kwenye machimbo na wenyewe waende kule wanakochimba wale watu. Wizara pia iliahidi kuwawezesha wachimbaji wadogo wadogo, nafahamu kwamba hii ni private sector, kuwapa mitaji mmoja mmoja ni vigumu, lakini ng’ombe anayekupa maziwa lazima umlishe, wenyewe wanakiri kwamba sekta ya madini ndiyo sekta inayolipa kuliko sekta nyingine yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde thelathini.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa faini aliyoitoza NEMC na Mheshimiwa Waziri kwenye Bonde la Mto Tigiti. Wametoza faini ya bilioni moja inaonekana ni kubwa, lakini kiuhalisia madhara makubwa yaliyopatikana kwa watu wale bado wanahitaji kulipwa fidia. Hatukubaliani kanda ya ziwa ndiyo inayoongoza… (Makofi)

SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye Wizara hii muhimu ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema kwamba nchi nyingi ambazo zimeendelea waliwekeza, Serikali ilitenga bajeti kubwa ilielekeza fedha nyingi kwenye Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ni Wizara ambayo ndiyo engine ndiyo ina uwezo wa kusisimua uchumi kwenye Wizara zingine nyingi kwa sababu wao ndiyo connection kati ya uchumi kwa maana ya uwekezaji na maendeleo ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2021 Tanzania waliingia kwenye Mkataba wa Umoja wa Afrika Mkataba unaitwa Africa Continental Free Trade Area, mwaka 2021 sisi ndiyo tulisaini. Kwenye mkataba huu katika nchi 55 ambazo ni wanachama nchi 54 zimeshasaini na lengo la huo mkataba ni kufungua biashara na huduma katika nchi za Afrika ambazo ni wanachama kutufungua ili tuweze kusafirisha biashara na kuepuka ushuru na gharama mbalimbali ambazo zinaweza kuwa ni vikwazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hivi kweli Tanzania tuko tayari kuanza kwenda kuuza kwenye hizo nchi zingine ambazo ni wanachama? Au ukiangalia kiuhalisia sisi ndiyo tutakuwa tunaletewa bidhaa kuliko kuuza huko nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma kwa mfano kwenye ripoti ya CAG ya mwaka 2022; SIDO ambao ni Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo Vidogo waliomba bajeti kwa ajili ya kuboresha mazingira ya uwekezaji wa viwanda vidogo vidogo. Kwenye bajeti waliyoomba ya shilingi bilioni 21 ili waweze kuendeleza maeneo hayo wamepewa shilingi bilioni 1.7 na kwa sababu hiyo asilimia 70 ya maeneo ambayo ya kimkakati walidhani watakwenda kuendeleza kwa ajili ya kuwekeza kwenye viwanda vidogo vidogo haikuendelezwa. Tafsiri yake ni kwamba Watanzania tumeshindwa kuwekeza kwenye viwanda hata kama Rais wa nchi akiwa na nia njema kiasi gani, akizunguka duniani kiasi gani kutafuta wawekezaji unufaikaji wa Watanzania kwenye eneo la viwanda na biashara ni ndoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2018/2019 hapa Bungeni kwenye Finance Bill tulihamisha Shirika linalosimamia ubora wa chakula tulilihamisha tukalirudisha TBS. Sasa TBS inakagua ubora wa matairi, TBS inakagua ubora wa matofali, TBS inakagua ubora sijui wa magari. TBS hiyo hiyo ianze kuangalia ubora wa maparachichi, TBS hiyo hiyo ianze kuangalia ubora wa matikitiki maji, tutafika kweli Na hiyo practice dunia nzima ubora wa chakula una kitengo chake idara yake maalum ambayo inatakiwa isimamie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kama tukitangaza vipi Tanzania kwamba tunaweza kwenda kuwekeza na Waziri anasema sasa hivi tunaweza kwenda kuuza mazao yetu nje, huwezi kuuza mazao ambayo yamezalishwa chini ya kiwango. Waziri anaongelea habari ya uzalishaji wa parachichi, alizeti kama haijapimwa, haijasimamiwa ina afya toxin nyingi hayo mahindi ukitaka kwenda kuuza nje mwisho wa siku yatazuiwa mpakani yatarudishwa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mwisho wa siku Tanzania rasilimali tuliyonayo wala hatuhitaji kuweka incentive, wala hatuhitaji kusema tunawavutia watu, Tanzania ina madini, mtu yeyote anayetaka kufanya biashara atakuja kuchukua madini Tanzania bila kujali kwamba umempunguzia ushuru kiasi gani, mtu yeyote anayefanya biashara atakuja kuchukua mazao Tanzania kwa sababu chakula ni hitaji muhimu kwa binadamu yeyote, lakini mwisho wa siku ni lazima Wizara ya Viwanda na Biashara ikasimame kama muhimili ambao unasaidia kufungua Watanzania wawekezaji wadogo wadogo na Serikali na mataifa ya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara hii ya Viwanda na Biashara ni Wizara nyeti sana, ndio Wizara ambayo inatakiwa iwe na wachumi na watafiti wanaoweza kuishauri Serikali uwekezaji wa kimkakati ambao unaleta tija kwa Taifa na unaongeza pato la Taifa. Pale kwangu Shinyanga Mjini wamejenga inaitwa machinjio ya kisasa, five billion za Serikali zimewekezwa pale wanasema wakati wanaleta huo mpango kwa bashasha wanasema wanawekeza bilioni tano kujenga yale machinjio ya kisasa kwa maana gani, kwa siku tutaweza kuchinja ng’ombe na mbuzi wasiopungua 500.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka wa tatu/wa nne sasa hivi ng’ombe wanaochinjwa pale hawafiki 15; five billion imewekezwa hiyo ni kazi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kuishauri Serikali uwekezaji wa kimkakati. Ukienda Kibaha kuna kiwanda pale Serikali imezika fedha billions of money kiwanda cha viuwadudu na kaka yangu ameeleza vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kile kiwanda pale Serikali imeweka fedha na viuwadudu hivyo vinavyotakiwa kuuwa malaria ni ugonjwa unaoongoza kuuwa Tanzania. Viuwadudu vinavyoweza kuuliwa na dawa ambazo zinazalishwa kwenye kiwanda kile ambacho tumeingia ubia na Cuba ni pamoja na wadudu wanaoleta malaria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekazana kununua neti, Serikali inatoa fedha nyingi kwenda kutibu watu na madawa tunajisifu kwamba tuna madawa na tumefungua hospitali kila kata, kila Kijiji, sijui kila nini, lakini kiuhalisia wale wadudu wangeweza kuteketezwa na hii ndio kazi ya Viwanda na Biashara, ndio maana hii Wizara imekuwa unpopular labda ni kwa sababu sijui haina fedha au haionekana kama ni Wizara ya muhimu, lakini sasa hivi ambapo Mheshimiwa Rais analeta uwekezaji ndani ya nchi Waheshimiwa Mawaziri mumsaidie kumshauri, ninyi ni cross cutting, ni Wizara mtambuka, mnauwezo wa kwenda kushauri kwenye kilimo, kwenye mifugo, kwenye afya, kwenye madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi Mheshimiwa Biteko wakati anajibu hotuba yangu niliyoongea kuhusu madini anasema anakwenda kuwasaidia wafanyabiashara wa madini wale wadogo wadogo kwa kuwapa mikopo na kuwaombea kwenye benki, lakini Wizara yako inatakiwa ijue Je, hiyo mikopo wanayopewa wawekezaji wadogo ina tija, wale watu wanaenda kupewa mikopo condition namba moja anatakiwa apeleke hati, sasa yule mchimbaji mdogo mdogo anayekaa kule Mwakitolyo mchimbaji mdogo mdogo wa Mwazimba sijui kule…, anatoa wapi hati ya nyumba ili aweze kupata mkopo? Uwekezaji mdogo anaambiwa riba atalipa kwa mwezi na riba ya kibiashara kama mtu aliyefungua duka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi ili niweze kupata madini lazima kwanza nianze kuchimba shimo, nifunge matimba, nivute maji nikimaliza kuvuta maji nianze kuchimba, nipeleke plant, niende nikachenjue, miezi tano, sita, saba, sasa miezi sita saba unamwambia huyu mfanyabiashara alipe riba kwa mwezi hiyo fedha anaitoa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kubwa ya Wizara ya Viwanda na Biashara ni kuangalia uwekezaji wenye tija na mimi nishauri Wizara hii itengeneze kamati maalum au timu maalum…

(Hapa kengele ililia kushiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Nami niungane na hoja ya Mheshimiwa Mbunge ya kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuimarisha demokrasia na sera ya mambo ya nje kwa maana ya foreign policy.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kusema kwamba nafikiri hatumuelewi vizuri Mheshimiwa Rais ukiniambia niseme kwa neno moja nitasema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni Balozi wa nchi za Afrika. Nitoe mfano mdogo, pamoja na mambo mengi aliyoyafanya, juzi alizungumzia kuhusiana na sheria iliyotungwa huko Marekani inayozipa nchi za Afrika fursa ya kupeleka bidhaa, huduma na utaalam kwenye nchi ya Marekani, hiyo sheria ilipitishwa mwaka 2000 na haijawahi kutekelezwa kwa miaka 23 sasa, lakini juzi Makamu wa Rais wa Marekani alipokuja Tanzania pamoja na kutembelea nchi zote Mheshimiwa Rais aliamua kusimama kwa Afrika, akaomba nchi za Afrika mkataba ule utekelezwe, pamoja na hilo pia aliomba Visa ya Watanzania kwenda Marekani iongezwe muda isiwe na ukomo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana ya Mheshimiwa Rais kuifungua Afrika au kuifungua Tanzania kwenye nchi za ulimwengu wa Kwanza ni kwamba Watanzania tuweze kwenda kupeleka bidhaa zetu kwenye nchi za ulimwengu wa Kwanza ikiwemo Marekani. Tupeleke utaalam wetu, tupeleke Wakandarasi wetu wakafanye kazi kule kama ambayo Wakandarasi na bidhaa za kule zinakuja Afrika.

Mheshimiwa Spika, sasa ili hayo mambo yaweze kutekelezeka kwa vitendo ni lazima tumsaidie Mheshimiwa Rais kuwaandaa watu wetu, kuandaa vyombo vyetu, kuandaa mazao yetu raw materials zote ziweze kupelekwa kwenye maeneo hayo. Sasa ili hayo yafanyike ni lazima Bunge na Serikali tushirikiane katika kuhakikisha taratibu, sheria, kanuni, mienendo na mfumo wa nchi unaweza kuwandaa Watanzania kukimbilia fursa hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi tunawezaje kupeleka wataalam wa kitanzania ambao wanaweza kwenda kufanyakazi kwenye nchi za ulimwengu wa kwanza, kama tangu Bunge hili mimi ninakaribia miaka Nane kwenye Bunge hili, tumeomba tubadilishe mitaala ili wanafunzi wetu waweze kwenda kufanya kazi katika nchi za nje mpaka leo mitaala haijabadilishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niliwahi kutoka agizo ndani ya Bunge hili tukufu kwamba vitabu vya kiingereza vyote vibadilishwe viwe vya Kiswahili, agizo hili lilitimizwa ndani ya miezi mitatu tu leo tuna miaka miwili ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mtaala wa Elimu wa Tanzania haujabadilika.

Mheshimiwa Spika, tunawezaje?

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Husna Sekiboko.

T A A R I F A

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Salome Makamba kwamba agizo la Mheshimiwa Rais la kuboresha mitaala limeshafanyika na hivi juzi Wizara ya Elimu imeipitisha Kamati kwenye mabadiliko hayo na muda siyo mrefu hata Bunge litapata fursa ya kuweza kupitishwa kwenye mabadiliko hayo, na kwa taarifa tu ni kwamba maboresho yaliyofanyika ni makubwa yenye tija kubwa kwa nchi yetu, tusubiri muda ufike tuyapitishe ili tuweze kunufaika na mabadiliko hayo.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo siipokei, habari ya kusema hivi karibuni, Bungeni humu taarifa bado haijaingia kwa hiyo ninavyozungumza hivi sasa
ni kwamba Bunge halijapitisha mtaala mpya wa Serikali unaohusiana na elimu, bado hatujapitisha hilo ni moja.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, tumejadili hapa kuhusiana na namna ya kutengeneza mazingira rafiki ya uwekezaji, tulipitisha habari ya blueprint economy, kwamba tuwe na one stop center kwa ajili ya kumsaidia Mwekezaji anapokuja Tanzania asihangaike kukimbia huku na kule, lilikuwa Azimio la Bunge Serikali mpaka leo hakuna yaliyotekelezwa.

Mheshimiwa Spika, tulipitisha kuhusiana na mabadiliko ya Sheria ya Habari ili tupate uhuru wa Vyombo vya Habari, sheria imeletwa vipande vipande, zote za Habari bado zinamapungufu jambo ambalo linatutia doa! Mmesema tuwaoneshe watu mlango wa kupitia hiyo ndiyo milango sasa nawaonyesha. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, Waziri wa Fedha...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuwapongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri. Ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ukurasa wa 21 na 22, ningependa kujikita hasa kwenye kuboresha mazingira ya uwekezaji na kuboresha mazingira ya wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbunge mwenzangu Mheshimiwa Mwambe aliomba Mwongozo asubuhi, lakini napenda nikazie hapo kwenye suala zima la kuboresha mazingira ya biashara na mazingira ya wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimuundo na kimfumo Serikali imejipanga vizuri sana kuhakikisha inawalinda wafanyabiashara wanaoendelea kufanya kazi na kuwakuza wafanyabiashara wadogo waweze kuingia sokoni na kushindana kiushindani. Kimuundo Serikali imeweka Tume ya Ushindani wa Kibiashara ambapo mtu yeyote anapodhani kwamba hapendezwi au hafurahishwi na mwenendo wa biashara sokoni kwa washindani wake, anaweza kwenda kupeleka malalamiko au anaweza kwenda kufanyiwa tathimini. Kama hataridhika shauri lake litapelekwa kwenye Mahakama ya Ushindani wa Kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuna jambo ambalo kidogo linaendelea ambalo linaweza kuleta shida kubwa sana ya biashara ya saruji nchini. Mwaka 2022 Kampuni ya Twiga Cement iliomba kwenda kununua hisa ya kampuni ya Tanga Cement. Baada ya kuomba Tume ya Ushindani ilikwenda kufanya tathimini kama sehemu ya majukumu yake. Kwa sababu moja kati ya sifa kubwa ya kuweza kununua hisa za kampuni nyingine ambayo mnafanya biashara inayofanana, hautakiwi kununua hisa kwa zaidi ya asilimia 34 ili usije ukalimiliki soko la biashara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tathmini ilipofanyika ya hisa za Tanga Cement kununuliwa na Twiga Cement ilionekana kuna uwezekano mkubwa baada ya kununua hisa zile, Kampuni ya Twiga Cement ingeweza kumiliki hisa zile zaidi ya asilimia 68. Pia Tume ikasema kwa hatari hiyo itaifanya Kampuni ya Twiga Cement kuwa kubwa iweze kumiliki lile soko, jambo ambalo lingeweza kuleta madhara kwenye upangaji wa bei kwa sababu yeye ndio mdau mkubwa kwenye eneo hilo. Ingeleta madhara makubwa kwenye upangaji wa bei, ingeleta madhara makubwa kwenye mfumuko wa bei lakini ingeleta gharama kubwa kwa mlaji ambao ni wanunuzi wa saruji yaani sisi wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maamuzi yale yalipotoka hawakuridhika nayo, wakaenda kwenye Mahakama. Mahakama ikakubaliana na maamuzi ya Tume wakasema Hapana, wasipewe kwa sababu watalimiliki soko la cement nchini, jambo ambalo linaweza likaleta madhara makubwa kwenye uchumi wa nchi hasa katika eneo la cement. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Tume imesema, kama Mahakama imeamua, juzi tarehe 23 Februari hapa, Tume imetangaza kwamba Twiga Cement wataendelea kununua hisa za Tanga Cement, maamuzi hayo wanayapata wapi? Nguvu hiyo wanaitoa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo madhara makubwa sana. Unajua mpaka sasa hivi tunapozungumza pamoja na viwanda vya cement kuwa vingi, bidhaa ya cement ina bei ya juu sana nchini. Kuna watu wananunua cement mpaka …

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi.

MHE. ELIBARIKI KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kingu hapa.

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Kingu utachangia muda si mrefu. Naomba u-reserve hiyo taarifa. Endelea Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Yapo madhara makubwa sana ya mmiliki mmoja kuwa na uwezo mkubwa wa kuamua bei, kuwa na uwezo mkubwa wa kupanga manunuzi na usafirishaji wa bidhaa ya cement hasa kwa wakati huu ambao nchi ndio inakwenda kujijenga kwenye maeneo ya viwanda, biashara na pesa nyingi za Serikali zinakwenda kwenye miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningeomba Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo inasimamia masuala haya ya uwekezaji, wajaribu ku- kulisimamia hili suala, kwa sababu mwisho wa siku mfumuko wa bei ukitokea kwenye cement, madhara ni yale yale ambayo tuliyaona kwenye sukari, kwenye mafuta ya kula na mambo mengine. Kwa hiyo ningeiomba sana Wizara itusaidie, ilimradi maamuzi yameshatolewa na Mahakama njia pekee ambayo Twiga Cement au haya makampuni yanaweza kufanya ili kumilikishana share ni kuomba marejeo ya maamuzi ya Mahakama ya Ushindani na sio kwenda kufanya ambavyo wanafanya. Kwa hiyo, naamini Serikali makini itakwenda kulisimamia hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nirudi kwangu Mkoa wa Shinyanga. Kitakwimu Mkoa wa Shinyanga unaongoza kwenye unyanyasaji wa kijinsia, mimba za utotoni na ndoa za utotoni. Ningeomba sana Ofisi ya Waziri Mkuu waifanye Shinyanga kama kanda maalum kwa ajili ya kutekeleza jambo hili. Asilimia 59 ya watoto waliopo Shinyanga wanaolewa wakiwa na umri wa chini ya miaka 18 na sielewi ni kwa nini Serikali imeamua kutumia nguvu yake kwenda kulirudisha nyuma suala la ndoa za utotoni ambalo limekwishaamuliwa na Mahakama kwamba tuletewe humu tubadilishe sheria, eti sasa hivi wanaenda kukusanya maoni ya wadau. Hii inaonesha ni jinsi gani sisi hatuko serious. Walete Sheria hapa tubadilishe na kama wanadhani kuna utaratibu umekiukwa au umekosewa tutajadili humu Bungeni hili ndilo jumba la Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha asilimia 44 ya wanawake walioko Shinyanga wananyanyaswa ndani ya ndoa zao. Manyanyaso mengi na ukatili mwingi wa kijinsia sasa hivi uko kwenye ndoa. Mwanaume anampiga mke wake anasema yule nikimpelekea kitenge na kanga atakausha hawezi Kwenda kulalamika. Manyanyaso mengi yanatokea ndani ya ndoa, Shinyanga hali ni mbaya. Ndoa za utotoni zimekithiri, mimba za utotoni zimekithiri, unyanyasaji wa kijinsia na sio wanawake tu. Ripoti iliyotoka mwaka 2022, walioripoti unyanyasaji wa kijinsia 42,245 walikuwa ni wananwake na 5,774 walikuwa ni wanaume. Kwa hiyo unyanyasaji uko pande zote mbili, elimu inatakiwa itolewe, kuweka dawati la jinsia peke yake haitoshi. Tuweke awareness kwenye jamii, tutoe elimu na watu wachukuliwe hatua. Mila na desturi mbovu ndizo zinafanya wanawake na watoto washindwe kuripoti mambo haya ya unyanyasaji wa kijinsia na ukatili wa kijinsia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali kama ambavyo kuna baadhi ya maeneo yamewekewa kanda maalum kwa sababu za kiusalama na Shinyanga iwekewe Kanda maalum kwa sababu ya unyanyasaji wa kijinsia. Kwa sababu ikitoka Shinyanga inafuata Tabora, ikitoka Tabora wanafuata wenzetu wa Mkoa wa Mara, unyanyasaji wa kijinsia kwa Kanda ya Ziwa hali ni mbaya sana na inachagizwa na mila potofu, utamaduni mbovu, kutokuelewa ambapo wananchi wengi bado wako kwenye hii changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie bajeti hii ya madini kwa mwaka 2023/2024. Nami niungane tu Wabunge wenzangu kuwapongeza Wizara kwa kazi nzuri ambayo wanafanya ya kusimamia sekta hii nyeti ya madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba tunajisifu kwamba tumefanikiwa sana kukusanya mapato kudhibiti wizi katika sekta ya madini bado tunalo jukumu moja kubwa la msingi ambalo hatujalitimiza la kuhakikisha maeneo au watu wanaoishi kwenye maeneo yenye madini wanafanana na thamani ya madini yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nitaliongelea kwa maeneo mawili tu kama maeno ya mfano eneo la kwanza ni eneo la fidia kwa watu ambao wanapisha wawekezaji wa maeneo ya madini. Hawa wananchi ukienda kufanya tathmini ya haraka, kabla hawajapisha maeneo yale walikuwa wana maisha mazuri wakishalipwa fidia ni kweli wanalipwa fedha nyingi lakini miaka kadhaa baada ya kulipwa fidia wale watu wanarudi kwenye ufukara na umaskini uliokithiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri Mheshimiwa Waziri atusaidie kwa sababu mwisho wa siku kumpisha Mwekezaji siyo lazima akulipe fidia peke yake, kwa nini Wizara isitengeneze mipango ya muda mrefu angalau hao watu wanaoishi kwenye maeneo ya madini waweze kupewa hisa nao wawe sehemu ya makampuni hayo ambayo yanawekeza. Jambo hili litawafanya hao watu wawe na pesa za muda mrefu, zitawafanya wawe na Maisha ya muda mrefu, itawafanya hata kama watapoteza fidia kidogo waliyopewa ile awali basi wanaweza kuendelea kuboresha uchumi wao kupitia hisa zile ambazo watakuwa wanalipwa mwaka hadi mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nilisisitize ni eneo linaitwa corporate social responsibility. Watu wanaoishi kwenye maeneo ya madini hawafanani, na mimi nimetoka Shinyanga, hawafanani na madini yanayochimbwa, hawafanani na utajiri ambao Mwenyezi Mungu ametujalia. Kwa mfano, ukienda Tarime pale tulienda juzi na Kamati yetu ya TAMISEMI wale watu wamepewa Bilioni Saba hela ya corporate social responsibility ile pesa waliyopewa ukifika pale hauoni matokeo ya Bilioni Saba kuingia katika Halmashauri ya Tarime huioni! Ukiuliza wanasema sisi Halmashauri sheria iko vizuri inaonesha kwamba Halmashauri lazima uishirikishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri inashirikishwa kwa maana ya kuchagua miradi ya kutekelezwa lakini Mkandarasi anayeenda kutekeleza mradi ule anaamuriwa na mgodi, aina ya class ya Mkandarasi na ujenzi wa jengo inaamuriwa na mgodi! Kama Serikali inaweza kujenga madarasa kwa Shilingi Milioni 20 ni kwa nini tumruhusu mgodi alete Mkandarasi ambaye anakuja kujenga shule ya aina ileile kwa gharama ya zaidi ya Milioni 500 kwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi…

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi?

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Waitara.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwita Waitara.

TAARIFA

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Salome Makamba kwamba anaendelea kuchangia vizuri lakini pia mimi ni Mjumbe mwenzake wa Kamati ya TAMISEMI, nadhani amechanganya maelezo Jimbo la Tarime Vijijini ambalo mimi ndiye Mbunge wake na Halmashauri tunaongoza, hizo shilingi bilioni 7.3 ambazo zimetolewa sasa hivi, ziko zinazunguka kwenye Kata 26 tunatumia Force Account siyo Mkandarasi kutoka mgodini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichofanyika fedha ambazo zilitolewa mwaka 2019/2020 wakati ule sikuwa Mbunge wala hatukuwa tunaongoza Halmashauri, shilingi bilioni 5.7 ndiyo ambazo alikuwa analipa Mkandarasi na miradi ina viporo mpaka leo, hilo ndilo ambalo lilielezwa kwa Kamati hiyo. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Salome Makamba unapokea taarifa?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona jamaa anadhani tunafanya kampeni hapa. Wamemsikia watu wa Tarime nashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa inayotolewa ya CSR sheria iko wazi Mheshimiwa Waziri tusaidie, Mkandarasi aamuliwe na Halmashauri na Force Account ndiyo iamue nani ajenge, nani alipwe, wakati gani na mradi gani utekelezwe ambao utaacha alama kwenye maeneo ambayo yana madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye suala la mikopo ya wachimbaji. Mheshimiwa Waziri mimi niliwahi kuchangia hapa nikakuomba sana uwasaidie wachimbaji wadogo wapate mikopo kwa sababu na wale wanafanya uwekezaji na wanachangia kwenye nchi hii. Mheshimiwa Waziri uliniahidi na kweli umeenda kuwapelekea mikopo, sasa mikopo uliyowapelekea Mheshimiwa hizo benki ulizowapelekea zinazotoa mikopo wanataka hati za nyumba, hizo benki wanaopelekewa mikopo riba zao ni za kibiashara, marejesho yao ni kwa mwezi, bado mazingira ni magumu sana kwa wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Serikali inalo fungu la pesa kwa ajili ya kuwasaidia wachimbaji wadogo, Serikali inakusanya pesa kupitia wachimbaji wadogo, ni kwa nini Serikali isitenge ruzuku kwa ajili ya kuwasaidia wachimbaji ili mwisho wa siku na wao waweze kuchangia katika Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukisema leo tunaenda kuwatoza, hawa wachimbaji wadogo tozo nyingi wanazotozwa wanatozwa katika mitaji yao, uwekezaji katika sekta ya uchimbaji mdogomdogo mtu anaweza akawekeza mpaka mwaka mpaka miezi miaka miwili lakini kodi analazimishwa kulipa kila mwezi, na Halmashauri kila siku inatunga sheria, utasikia sijua Afisa Biashara anataka kodi, Afisa Mazingira anataka kodi, mlundikano wa kodi ni mkubwa sana. Tusiwape mikopo ya kibiashara wachimbaji wadogo hatuwasaidii, tunawanyonya ndiyo maana watu wanaishia kukwama huku wanatelekeza famila zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye masuala ya mabwawa ya matope na mabwawa ya sumu. Nchi hii ilichafuka sana kipindi cha nyuma kule kwenye Mgodi wa Barrick wa Nyamongo, bwawa lilipasuka la sumu na watu wakapata madhara, tukapelekwa Mahakamani tukashitakiwa na nini na hekaheka zikawa nyingi sana. Juzi pale Mwadui bwawa la tope limepasuka pia, tunamshukuru Mungu madhara hayakuwa makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi ningeomba nipendekeze Serikali ifanye tathmini ya haya mabwawa mara kwa mara, kwa maana ya kwamba iwe angalau kila baada ya Miezi Sita Serikali ipite ifanye tathmini ili kuhakikisha kwamba mabwawa haya ni salama kwa maisha ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa Serikali inapokuja kujibu inipe majibu, maana mimi ni Mbunge ninatokea Shinyanga lakini sijaipata ripoti ya tathmini ya madhara ya kupasuka kwa bwawa la tope la Mwadui, ninataka nijue ushiriki wa Serikali katika kufanya tathmini, ushiriki wa Serikali katika kutoa fidia na kuwarejesha wale watu katika maisha yao bora kuliko walivyokuwa zamani. Kwa sababu lile bwawa lilipasuka tope lilifunika nyumba, mali zilipotea, sasa nataka nijue nini ilikuwa ushiriki wa Serikali katika kudhibiti kupasuka kwa bwawa la tope la Mwadui na compensation waliyopewa wale watu, tathmini ilifanyikaje ningetamani sana kupata majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa yote naendelea kusisitiza kwa Mheshimiwa Waziri anakusanya mapato, anachangia kwenye bajeti ya Serikali lakini na sisi wananchi kutoka kwenye maeneo ya uchimbaji, tunataka tufanane na rasilimali zilizoko katika maeneo yetu, fidia peke yake haitoshi tunataka tulipwe fidia lakini tuwe sehemu ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana leo mwekezaji anajenga shule anajenga vituo vya afya mwisho wa siku watu wana vandalize kwa sababu mtu anaona hiki ni kituo cha afya cha mwekezaji, hiki ni kituo cha afya cha mgodi, lakini kama mimi mwananchi ninayetoka Shinyanga ninayetoka Kakola ninayetoka Mwadui nitaona kwamba huu mgodi ni sehemu ya mimi na unaninufaisha lazima nilinde rasilimali zote ambazo zinajengwa na mgodi, lazima nilinde mali zote ambazo tunajenga mimi pamoja na mgodi nikiwa kama sehemu ya uwekezaji wa mwekezaji huyo. Baada ya kusema hayo nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Tarehe 13 Mei, 2022 niliuliza swali hapa Bungeni juu ya Makampuni ya simu kukata muda wa maongezi wa watanzania ambao haujatumika kwa maana kwamba bundle lime-expire. Na Waziri wakati ananijibu alisema kwamba wameelekeza Makampuni ya simu mtu kama bundle lake lime-expire basi akinunua bundle lingine ule muda uliyopita arudishiwe. Hiyo ninahesabu kama ni dhulma kwa watanzania kama ndivyo wanavyofanya basi Mheshimiwa Waziri haujatenda haki kwa watanzania.

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jackson Kiswaga, taarifa.

T A A R I F A

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nataka niweke sawa jambo hili kwamba ukizungumzia bundle linakuwa limited kama ni siku 30 kama ni siku 15. Lakini nafurahia Waziri alisema kwamba kama ukiongeza linavyokaribia kwisha unaongezea muda wa mazungumzo. Kwa hiyo ndiyo business model yaani ndiyo biashara iko namna hiyo. Ahsante sana.

MWENYEKITI: Kwa hiyo ndiyo taarifa. Mheshimiwa Salome unapokea taarifa?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei na namshauri Mheshimiwa Mbunge atulie, asubiri nifafanue. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kasema clear hapa kwamba watanzania asilimia 95 wana-access ya mtandao kwa maana ya kwamba wana-access ya minara ya simu. Kwa hiyo, wanaweza kutumia simu, kwa maana hiyo wanaweza kujiunga kwenye vifurushi vya kupiga simu. Na amesema asilimia 68 ya watanzania wanauwezo wa kujiunga kwenye vifurishi vya internet yaani wanaweza kupata access ya internet.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, ukijiunga kwenye kifurushi cha internet au bundle lile bundle unatakiwa ulitumie ndani ya siku moja. Ikitokea kwa namna yoyote ambazo mara nyingi mtu anashindwa kutumia bundle lile kwa sababu ya kukosa mtandao kwa sababu maeneo mengi bado hayana access ya mtandao au anashindwa kutumia bundle lile kwa sababu ya changamoto za kampuni za simu. Kwa sababu hizo sasa yule mtu ambaye bundle lake lime-expire hawezi kurudishiwa hiyo pesa ambayo ime-expire. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa mantiki hiyo, kama mtu yule analazimishwa ili arudishiwe ile pesa yake ambayo ime-expire ni lazima ajiunge dakika chache kabla yaku-expire kwa bundle lile au muda wake wa maongezi kama analazimishwa kufanya hivyo ni kumlazimisha mtu kufanya matumizi ambayo hakuyapanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, makampuni ya simu yakifanikiwa kukata shilingi 200 tu kwa watanzania Milioni 50 ambao Mheshimiwa Waziri amesema, wakifanikiwa kukata shilingi 200 tu kwa siku kwa maana ya kwamba bando lime-expire au kifurushi cha muda wa maongezi kime-expire kwa siku moja wanauwezo wa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 10. Kwa mwezi wanakusanya zaidi ya bilioni 300. Mheshimiwa Waziri hapa ameomba hapa hela anayoomba kwa ajili ya Wizara yake, ameomba shilingi bilioni 282. Kwa hiyo, pesa hiyo wanaweza kukusanyia ndani ya mwezi mmoja tu wakakupatia na ukafanya kazi za Wizara yako zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuwe makini sana. Bilioni 300 za watanzania zinaweza kupotea ndani ya mwezi mmoja kwa sababu ya bundle lime-expire au muda wa maongezi umeisha muda wake na wakati siyo kosa la watanzania kushindwa kutumia muda wa maongezi. Kusema kwamba hiyo ni biashara, biashara ni nguvu ya negotiation na kazi kubwa ya Wizara ni kuwalinda watanzania wasiibiwe na makampuni ya simu. Na Mheshimiwa Mbunge ananipa taarifa, kwa taarifa yake na mimi nimpe taarifa, hiyo biashara ya bundle ku-expire huko duniani ilishapitwa na wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zilizoendelea hakuna biashara ya bundle ku-expire. Nchi zinazoendelea hakuna biashara ya bundle ku-expire. Kwa nini Tanzania tunaruhusu makampuni ya simu yaibe pesa za watanzania kwa sababu bundle lime-expire? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana Mheshimiwa Bashe kwenye Wizara ya Kilimo wakati anaomba hela, ameomba bilioni 750. Hiyo pesa makampuni ya simu yanakusanya ndani ya miezi mitatu tu. Miezi mitatu tu wanakusanya, sisi tunatafuta mwaka mzima wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Wizara tunayo sheria ya kulinda mlaji (Consumer Protection Act) na kazi ya Sheria ile ni kumlinda mtanzania asiibiwe ambaye anatumia bidhaa hii ya simu na mtandao. Mheshimiwa Waziri anatakiwa kuacha legacy kwenye hili na ataacha legacy kama atahakikisha kwamba anawalinda watanzania waweze kutumia pesa yao ambayo wamenunua bundle au wamenunua muda wa maongezi bila bundle lile kuharibika. Na ukisema bundle lime-expire umeshusha thamani ya pesa ya Tanzania. Kwa sababu kama pesa yangu mimi shilingi 2,000…

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: ...iko mfukoni haijaexpire, ina-expire vipi pesa ambayo iko kwenye simu? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 5) wa Mwaka 2017
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba nami nichangie Muswada huu kwa kifupi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipende kumshauri Waziri mwenye dhamana kwamba muda uliowekwa kwa ajili ya kutoa taarifa ya kuendeleza ardhi kwenye Sheria ya Mabadiliko ya Ardhi wa miezi sita ni mchache sana. Sote tunafahamu kwamba lengo la mkopo ni kufanya biashara, sheria imelazimisha mtu achukue mkopo na aende akaendeleze eneo ambalo amekopea, kitu ambacho kwangu naona si sahihi kwa sababu akiwekeza au akiendeleza eneo lile inawezekana haikuwa malengo ya mkopo ule na hivyo anaweza akashindwa kurejesha, jambo ambalo linaweza likasababisha akanyang’anywa ardhi pia na hiyo financial institution.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niseme, ama kifungu hiki kiangaliwe kwa umakini zaidi au kama itawezekana muda wa kutoa taarifa ya uendelezaji uongezwe ili yule mtu aweze kuiwekeza ile pesa kwenye eneo lile kwa awamu ndogo ndogo wakati anakamilisha malengo yake ya kuchukua mkopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, niseme kuna mkinzano mkubwa sana kati ya Sheria ya Uendeshaji wa Mabenki Tanzania na sheria hii kwa sababu benki hazitoi mkopo kwa ardhi ambayo haijaendelezwa. Kwa sababu hiyo, ni lazima ili tuweze kupata maelewano kati ya sheria hizi mbili, Serikali ione umuhimu wa kuongea na watu wa benki waelewe nini lilikuwa lengo la kuweka sheria hii ili inapofikia kwamba wanatakiwa kuwakopesha watu ambao hawajaendeleza ardhi, pesa ziweze kutolewa kwa watu wale kama ambavyo sheria inaeleza, lakini mpaka sasa bado kuna ukinzani mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitoe mawazo yangu kwenye huu Muswada wa Utumishi wa Umma. Nadhani wadau katika Muswada huu hawajashirikishwa vizuri. Serikali imefikia maamuzi ya kuongeza kuanzia miaka 60 kwa hiari
na miaka 65 kwa lazima lakini bado ipo haja kubwa sana ya kuweza kuangalia maoni ya wadau. Kwa sababu kuna mafunzo mbalimbali yatatoka hapo watapewa wale wataalam ambao wamefikisha miaka 65, tunadhani yatafanyika kwa ufanisi na wakati mtu huyu tayari ana umri mkubwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiachana na hilo; unadhani kwa kuongeza mkataba, kwamba mtu atastaafu kwa miaka 65 kwa lazima, unadhani ndiyo inaleta ufanisi au unamlazimisha yule mtu afanye kazi hata kama hataki? Ndiyo tunarudi kwenye suala la morale; professionalism inakwenda na morale. Kwa hiyo nimshauri sana Mheshimiwa Waziri akazungumze vizuri na wadau kuhusu kuongeza umri, kwa sababu mimi naamini si wote ambao wanapendezwa na suala la kuongezwa umri wa kustaafu kama ambavyo imeelezwa katika proposal hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, nimalizie kwa kusema kwamba hii Sheria ya Ardhi kuna jambo la msingi ambalo tumelikwepa la zile ardhi ambazo zinamilikiwa kimila; bado nahitaji ufafanuzi kutoka kwa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana. Anasema wale wanaomiliki kimila, mabadiliko ya sheria hii hayatawagusa, lakini wapo watu wanamiliki maekari ya ardhi kimila na wanatamani kufanya uwekezaji kwa kuchukua mikopo; na hizi ndiyo zimekuwa kelele za Wabunge wengi humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi ardhi zao wanamiliki kimila na si kwa utaratibu wa Serikali na wakati mwingine sio kwa kutaka kwao, ni kwa sababu mfumo wa kupata hatimiliki ya Kiserikali bado haujakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri aliangalie suala hili la wale wanaomiliki zile hati kimila; naamini ipo sababu ya msingi kama kweli tunataka kufanya uwekezaji wa ndani, kama kweli tunataka kujenga Tanzania ya viwanda na kuwapa uwezo watu ambao wanawekeza, ipo sababu ya kuzingatia umiliki wa kimila. (

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Usuluhishi wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie muswada huu muhimu kwa taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kanuni za Kudumu za Bunge zinaipa mamlaka Kamati ya Bunge kushauriana na Serikali juu ya mambo mbalimbali kwa niaba ya Bunge zima.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Sheria Ndogo. Sheria hii imeletwa kwenye kamati yetu tuna kama siku 14 hivi; na tangu imeletwa kwenye Kamati moja kati ya mambo ambayo yalikuwa ni mabishano makubwa kwenye Kamati ni kujumlisha Sheria ya Usuluhishi pamoja na mabadiliko madogo ya sheria mbalimbali nne ndani ya muswada huu na kulazimisha ziingie ndani ya Bunge hili kwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Kamati imesomwa, yapo mambo ambayo yapo kwenye mabadiliko madogo ya sheria hizi nne ambazo Kamati ilikuwa ina hoja za msingi kuyakataa. Kamati ilitaka ipate muda zaidi ya kuyapitia mambo hayo ili iweze kujiridhisha kama zamu hii hatuji kufanya zoezi la majaribio kwa kupitia sheria ambazo baadaye zitarudishwa tena hapa ndani ya miezi michache kwa ajili ya kupitiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano mdogo tu katika hii part 13 ya Muswada huu wa Sheria ambayo inabadilisha hii sheria inayohusiana na Permanent Sovereignty kwenye rasilimali za taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika mwaka 2017 ndani ya Bunge lako ililetwa miswada 3 kwa hati ya dharura; na tukasema, miswada hii ina maslahi mapana kwa nchi yetu. Tanzania sio kisiwa tumeridhia mikataba mbalimbali duniani. Tukasema ni lazima ijadiliwe kwa maslahi mapana ya nchi yetu na kwa kuzingatia mikataba ya kimataifa tukaambiwa sisi tunatetea mabeberu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa moja kati ya kitu kilichopitishwa katika miswada ile ni Kifungu cha 11 cha Sheria ambacho leo kinakuja kufanyiwa marekebisho. Kwamba chochote kinachohusika na usuluhishi au kusikiliza kesi za mikataba ni lazima kiwe kimeanzishwa kwa mujibu wa Sheria za Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, wameenda ku-test haifanyi kazi kwa sababu tunayo ICC iko Arusha pale ni tribunal ya Kimataifa haijaanzishwa kwa Sheria za Tanzania. Sasa leo wamerudi kwa dirisha la mlango wa pili wameleta hii sheria ya usuluhishi wanataka kufuta hiyo kwamba lazima ianzishwe na sheria za Tanzania ili kuruhusu international arbitration ziweze kufanya kazi Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema Serikali kutumia dirisha la hati ya dharura kunaweza kuleta sheria mbovu ndani ya nchi hii, na mfano mzuri huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua hii inatokana na mkataba wa juzi ambao Mheshimiwa Kabudi ameingia na Barrick, inayoitwa Twiga leo, tunajua. Hebu angalia, leo wametubadilishia sheria hii lakini Sheria ya Natural Wealth and Resources Contract Review and Negotiation of Unquestionable Terms ya mwaka huo 2017 inasema Serikali inapoingia mkataba wowote wa kimataifa ni lazima ndani ya siku 6 za Bunge hili tulete mkataba huu hapa; umeletwa lini? Mkataba haujaletwa, na sisi kama Bunge tuna uwezo wa kuishauri Serikali kwamba mkataba huu si mzuri hauna maslahi kwa Watanzania Serikali mwende mka-renegotiate ili mlete mkataba wenye maslahi mapana na kulinda rasilimali za Tanzania. Lakini Serikali mpaka leo, tunasikia kwenye corridor tu mara tuna 16% mara tutagawana faida 50 kwa 50, kwa mtaji upi tulioweka?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo haya mambo hayafanyiki kwa bahati mbaya. Sisi tuliambiwa kwamba tunatumwa na mabeberu, tumepewa hela ndio maana tunangangania sheria za kizalendo za kutunza rasilimali za nchi zisifike ndani ya Bunge hili kwa hati ya dharura, tuliambiwa hivyo. Mimi nilizimiwa mic humu ndani, lakini leo wamerudi haifanyi kazi. Once again wamerudi hapa na arbitration act, tena wanatamba kweli kwamba hii arbitration act ina miaka mingi tangia mwaka 1932 unajua lazima tuibadilishe tunawaambia sawa ilikuja na mkoloni mwaka 1932 je, hudhani kwamba lazima tuibadilishe arbitration act kwa kuanza na sera ili iweze kuwa na muktadha na mahitaji ya Watanzania katika mambo ya migogoro ya kisiasa, kijamii, kuichumi, mjumlishe vyote i-accommodate the context ya Tanzani? Hawana majibu Mheshimiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kengele imeshagonga na nimekuachia hapo dakika ili umalize sentensi.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 3) wa Mwaka 2019
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nianze kwa kuwakumbusha Wabunge wenzangu kwamba, ndani ya Bunge hili tuko Wabunge 395, kama sijakosea, lakini leo tumeletewa sheria tisa. Kazi ya kwanza ya Bunge kwa mujibu wa Katiba ni Kutunga Sheria, ndio kazi yetu ya kwanza. Sasa katika Wabunge 395 leo tumeletewa sheria tisa ambazo tutazijadili kuanzia saa 4.00 kamili mpaka Saa 7.00 kamili, saa nne tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mjadala huo CCM wamepewa nafasi Wabunge wasiozidi kumi au kumi na mbili, CHADEMA wamepewa Wabunge wawili, ACT hajapewa hata Mbunge mmoja, CUF imepewa nafasi moja, NCCR hawajapewa nafasi. Mheshimiwa Zitto amelazimika kupewa nafasi moja ya CHADEMA ili na yeye aweze kutoa mchango kwa niaba ya ACT Wazalendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niseme hivi naheshimu sana mchango mkubwa uliofanywa na wenzetu walioko kwenye Kamati ya Katiba na Sheria.

MHE. JULIUS K. LAIZER: Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …kwa sababu wamejitahidi kadiri ya uwezo wao kufanya kazi mpaka Jumapili kuweza kupata maoni ya wadau.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu nimpe mzungumzaji Taarifa kwamba, kinacho- determine kiwango cha Wabunge kuchangia ni idadi ya Wabunge kulingana na vyama. Kwa hiyo, hakuna upendeleo, wanachangia kulingana na idadi yao. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, angenisikiliza tu angenielewa, twende polepole.

Mheshimiwa Naibu Spika, naheshimu mchango mkubwa wa Kamati ya Katiba na Sheria kufanya kazi mpaka Jumapili kuweza kujadili sheria hizi tisa, lakini Kamati ya Katiba na Sheria haizidi Wabunge 25, wako kama 25 hivi, haifiki hata robo ya Wabunge wote tulioko humu ndani. Sasa kwa mazingira haya ninayoyasema mimi tunawezaje kuepuka kuitwa kwamba, sisi Wabunge tumekuja kuidhinisha mapendekezo ya Serikali na sio kuyajadili? Tunawezaje kuepuka… (Makofi)

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …hiyo, kama kama jambo la muhimu…

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mhweshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …sheria za muhimu ninazokwenda kuzichambua sasa hivi zinaidhinishwa na Bunge hili badala ya kujadiliwa kama ambavyo Bunge linataka? (Makofi)

NAIBU SPIKA: Naomba ukae kidogo, Mheshimiwa Salome Makamba naomba ukae kidogo, Mheshimiwa Amina Mollel pia naomba ukae kidogo.

Mheshimiwa Salome Makamba nimetoa maelezo kwa kirefu. Ukizungumza wewe kama Mbunge kwamba, Bunge hili zima kama ulivyosema la Wabunge 393 ambalo wewe ni mmojawapo limekuja hapa ili liidhinishe kilicholetwa na Serikali, kule Kamati inafanya kazi gani? Muda wote ambao Kamati, wewe mwenyewe umekiri hapo ilikuwa inakesha, ilikuwa inakesha ikifanya nini na marekebisho yaliyoletwa na Serikali ni nani ameiambia? (Makofi)

Hii sheria tunayotunga hapa ni Bunge limetunga sio Serikali, Serikali ilishatoka kwao. Kwa hiyo, hiyo hoja ya Bunge kwamba, linakuja hapa kuidhinisha, Mheshimiwa Salome tuko hapa Bungeni na sisi kama taasisi tunafanya kazi yetu. Maoni yako yanaruhusiwa, lakini hapa ndani toa maoni yanayofuata utaratibu; maoni yako ukishatoka nje ya hili jengo unaweza kusema chochote kwa sababu, unaweza ukasema kwa mazingira haya mimi sio Mbunge, kule kaseme, lakini hapa ndani hilo sitaruhusu kwa sababu, mimi mwenyewe unanifanya ni sehemu ya chombo kinachoidhinisha mambo yaliyoletwa na Serikali wakati Bunge hili limekaa tangu, wewe mwenyewe ulivyosema hapo, ni muda gani Kamati imefanya kazi kwa niaba ya Bunge? Sasa wanafanya kazi gani?

Hakuna namna ambayo Bunge hili kanuni zetu zimesema zimeelekeza kwamba, Bunge hili litafanya kazi kwa kutumia Kamati, sasa wewe unataka kuiletea dharau Kamati ya watu ishirini sijui na nane, sijui shirini na ngapi kwamba, wao kule hawajafanya kazi yoyote isipokuwa humu ndani ndio tungefanya kazi kubwa, hapana, si sawasawa.

Endelea na mchango wako, habari ya Bunge kuidhinisha ya Serikali haipo. (Makofi)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, tunabishana kwa hoja tu, ni hoja tu. Mimi nimetoa hoja yangu, kama haitakubaliwa ni sawa, tunabishana kwa hoja na nitaendelea. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Hiyo ya kwako sio hoja Mheshimiwa Salome. Tukae vizuri tu, sio hoja kwa sababu, Bunge hili huwezi wewe kwa mawazo yako ukaliweka kwa namna ambayo unataka kuonesha watu wote hatufanyi kazi, hapana. Kama hamfanyi ama wewe hukupata nafasi ya kufanya hiyo kazi, basi Kamati imepata nafasi ya kufanya kazi kwa niaba ya Bunge na sisi hapa leo tumeisikiliza Kamati inasema nini na tunatumia hayo maoni ya Kamati kuishauri Serikali. Ndicho tunachokifanya hapa ndani, lakini kama wewe ama na wengine wote hawajafanya kazi yao, halilifanyi Bunge kwamba, halijafanya kazi yake, hapana. (Makofi)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba unitunzie muda wangu, Watanzania wataamua kama tumefanya Bunge au amefanya nani.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome, naona leo umejiandaa sana kubishana, naomba ukae. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie Muswada huu muhimu wa kubadilisha lugha za kisheria na Mahakama katika nchi yetu kuwa Kiswahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ieleweke kwenye Bunge lako tukufu kwamba hakuna mtu anayepinga kutumia lugha ya Kiswahili kwenye mahakama; hakuna na hata sheria yenyewe inayobadilishwa, Cap 1 ilisema kabisa. Kifungu cha 84 nitajitahidi kutumia Kiswahili kwa sababu tunabadilisha Kiswahili. Kifungu cha 84 kinasema kugha ya sheria za Tanzania itakuwa Kiingereza au Kiswahili au vyote; kwa hiyo hakuna anayepinga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, isipokuwa, kikubwa ambacho mimi nataka nishauri; Mwalimu Nyerere mwaka 1983 alitamani lugha iwe Kiswahili tu. Na baada ya kufanya hivyo, pamoja na mamlaka aliyokuwa nayo hakukimbilia kusema wote tuzungumze Kiswahili mahakamani. Alikwenda kwenye kubadilisha kamusi, tupate kamusi ya Kiswahili yenye maneno ya kisheria, itakayotumika kwenye sheria. Akaenda tukajaribu kufanya hivyo na mpango ule uli-fail.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ambacho mimi nataka nishauri Bunge hili tukufu; ni lazima tujitathmini, kwa hatua ya sasa, je, tupo tayari kubadilisha lugha ya Mahakama na lugha ya sheria iwe Kiswahili peke yake? Hasa ikizingatiwa kuwa tunayo changamoto kubwa sana ya namna ya kutohoa maneno ya Kiswahili ili yaweze ku-fit kwenye lugha ambayo tunaitumia ya Kiingereza ambayo imeshapimwa, imeshakuwa tested and well…, imeshapimwa na ikathibitika kwamba maneno yale yako sahihi. Najaribu kutumia maneno mazuri ya Kiswahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna changamoto kubwa, changamoto ya kwanza ni kwamba Tanzania siyo kisiwa na hatuwezi kusema tunaweza kusimama kama kisiwa. Mimi nilipokwenda kwenye Kamati niliwauliza; hivi ni nchi gani ambayo inatumia lugha yake ya asili katika mambo haya ya kimahakama? Sasa mifano ambayo tunapewa kwenye Kamati wanasema kuna nchi kama Finland, Ireland na Hong Kong.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi nchi population yake ni chini ya milioni 10. Wana uwezo hata wa kuwaajiri watu wake wote na wasipate ombwe la ajira. Sisi tunalazimisha tutumie Kiswahili halafu tumejadili hapa wiki nzima tuna changamoto ya ajira ndani ya Tanzania, tunataka tutumie Kiswahili kwenye mahakama zetu. Sasa hivi tu tunatumia Kiingereza kwenye Mahakama, Mawakili wetu Chief Justice anasema hawajui Kiingereza kwenda kwenye Mahakama nyingine za nje. Sasa pata picha tumetumia Kiswahili mwanzo mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mitaala yetu tunafundishwa kwa Kiingereza, kuanzia form one mpaka chuo kikuu ni lazima usome Kiingereza. Ukifika kwenye Mahakama kwenye ku- practice unaambiwa utumie Kiswahili. Ni lazima tufanye maandalizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati yenyewe imekiri walijaribu kutafsiri sheria ziende Kiswahili wame-fail. Kamati yenyewe inakiri Law Revision Commission (Tume ya Mabadiliko ya Sheria) kwa mara ya mwisho imefanya kazi mwaka 2002, miaka 19 iliyopita, hawajafanya…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba, kuna Taarifa. Mheshimiwa Agness Mathew Marwa. Zima kwanza hiyo ya mwanzo uliyokuwa umebonyeza.

T A A R I F A

MHE. AGNESS M. MARWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampa taarifa muongeaji kwamba anasema Kiswahili kinalazimishwa kubadilishwa, je, wapiga kura wake walimpigia kura kwa Kiingereza? (Kicheko/Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Salome Makamba.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba niendelee na hii ndiyo changamoto tuliyonayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sheria kuna kitu kinaitwa jurisprudence of law. Tunao majaji ambao wanatoa hukumu nzuri kweli kweli ambazo zinatumika kwenye common law, kwenye nchi mbalimbali. Hukumu hizi zinapokwenda kutumika kule zinakuza tasnia ya sheria katika nchi yetu. Sisi tumekomaa tunataka hizi hukumu zitoke za Kiswahili. Sasa tunataka tusonge mbele kwenye tasnia ya sheria kiuchumi, wakati huo huo tunataka tukuze Kiswahili kwa sababu ni uzalendo, tunu za taifa, yaani hatujui tunataka nini kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua ukiwa mzalendo halafu hauna uchumi, ni sawasawa na kuwa mwanaume mwenye ndevu halafu haumiliki uchumi, yaani hauna hela. Unakuwa tu kama Mzee Kambale, yaani una ndevu, una masharubu lakini mwisho wa siku haumiliki uchumi wa dunia. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo China inaheshimiwa kwa sababu uchumi wake uko imara, kila mtu anang’ang’ania…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: …kujifunza Kichina kwa sababu kujua Kichina ni uchumi.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, muda wako umekwisha Mheshimiwa Salome Makamba, ahsante sana.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
THE WRITTEN LAWS (MISCELLANEOUS AMENDMENTS) (NO. 4) ACT, 2021
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Huduma za Jamii, napenda kukufahamisha kwamba, MSD imeshaanza kuzalisha madawa. Hili walilileta kwenye Kamati na mimi ndiye niliyewa-guide nikawaambia kama mnataka kufanya production ya madawa lazima mlete Bungeni marekebisho ya sheria tuwape ruhusa ya kufanya kazi hiyo.

SPIKA: Sasa mbona humwambii jirani yako kwamba, mimi ndiyo nilitaka hili? Mheshimiwa Salome tuendelee. (Kicheko)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa sababu ya muda naomba niendelee pale alipoishia Wakili Msomi Mheshimiwa Agnesta kwa kuongelea mambo makubwa mawili. (Kicheko)

SPIKA: Najua mnanichokoza tu, leo sisemi. (Kicheko)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kwa kuongelea mambo makubwa mawili. Kwanza Part 7 ya Muswada imeongelea mambo ya Bima ya Afya, lakini wameongea vizuri na mimi kwa kweli siyo siri, niseme tu wamechukua maoni ya Wabunge kwa kuongeza umri wa watoto kutoka miaka 18 mpaka miaka 21 ukisoma Kifungu cha 37.

Mheshimiwa Spika, lakini nataka nikukumbushe kwenye Bunge lako hili, Bunge lililopita tulikubaliana na Waziri Mheshimiwa Jenista aliji-commit kwamba, kwenye Bunge hili wataleta Muswada wa Mabadiliko ya Sheria ya Bima ya Afya, wakasema watakuja tutajadili yale ambayo tunayahitaji yatakuwa accommodated na tutafanya mabadiliko makubwa.

Mheshimiwa Spika, maombi ya Wabunge ukienda kwenye Hansard, kwenye suala la Bima ya Afya hayako kwenye umri peke yake. Familia nyingi za Wabunge humu ndani hata wananchi tunaishi familia ambazo wategemezi wakubwa ni wazazi wetu. Tunawezaje kuwahudumia wazazi wetu kwa kutoa pesa ya mfukoni badala ya wazazi wetu kuwa-covered na Bima ya Afya?

Mheshimiwa Spika, wewe menyewe unafahamu Wabunge wengi humu ndani kama ana watoto wengi, labda mmoja, wawili na wengi ni vijana. Bima zetu za afya tunazokatwa hazijumuishi wazazi wetu, matokeo yake tunajikuta tunalipa hale nyingi na hatutibiwi na Bima ya Afya badala yake tunatoa hela za mfukoni kuuguza wazazi wetu. Hiyo ndiyo scenario ya Watanzania wote kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo wameleta kipande kidogo sana. Sawa ni cha muhimu, lakini walete Muswada kama walivyoahidi Bunge lako Tukufu.

SPIKA: Mheshimiwa Salome ukisema hivyo, wale wasiotutakia mema watasema Wabunge wanataka na Babu zao nao waanze kutibiwa kwenye Bima ya Afya, lakini hoja yako ni nzuri sana, kinachotakiwa kusema ni kwamba, hivi sasa watumishi wengine wa Serikali inaruhusiwa wazazi wao kuwemo katika Bima ya Afya. Kwa hiyo, ni vizuri na wengine nao waliomo katika hiyo mifumo ya Bima ya Afya wakahusianishwa pia. Nakubaliana na wewe, Naliweka tu vizuri, ili mwenye nia mbaya asije akasema tofauti. (Makofi)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, kwa maneno hayo uliyoyasema naomba yachukuliwe hivyo kwenye Hansard. Kwamba, Bima ya Afya i-accommodate wategemezi wakubwa ambao ndiyo wazazi tunaowalea familia nyingi za Watanzania, nakubaliana na wewe, hilo ni moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili. Wameleta Sheria kwenye Part 6 ya Muswada, Section 30, wanasema habari ya kuiingiza VETA kwenye NACTE, wanazungumzia generally.

Mheshimiwa Spika, angalia Part Six. Nakimbizana na muda.

SPIKA: 36?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, Part Six, Section 30.

SPIKA: 30?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

SPIKA: Mmhh, endelea.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, wanaongelea generally kuichukua VETA kuiingiza kwenye Mfumo wa NACTE. Narudi palepale na ulinipanga kwenye Kamati ya Huduma za Jamii kwa maksudi, ombi kubwa na lalamiko kubwa la Wajumbe wa Kamati ambao ndiyo wanawakilisha Idara hii ni kutaka wanafunzi wa VETA ambao ndio wengi, mafundi mchundo na wengine, wapate mikopo ili waweze kusoma kirahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hicho ndio kilio kikubwa na siyo muundo, wala Board of Directors, wala nini. Kilio kikubwa wanafunzi wa VETA, Serikali inajinasibu kwamba inaenda kwenye Tanzania ya viwanda, ukiangalia kwenye pyramid ya ajira walio wengi ni watu wa vocational, mafundi, technicians, wale wanaenda chuo hawapati mkopo.

Mheshimiwa Spika, nimeona Mheshimiwa Waziri Mkuu anajitahidi kufungua Vyuo vya VETA huko mitaani. Sasa wasipopata mkopo hawa watu wanashindwa kusoma tunakosa technicians. Hawa watu wanatuletea vitu vipande- vipande kuna tatizo la msingi hapa, ni lazima hili tatizo lihudumiwe.

Mheshimiwa Spika, nadhani hilo nimeeleweka. Niende kwenye sehemu ya mwisho na hili ni muhimu sana tujadili…

SPIKA: Hili umeleta amendment au hii hukuleta?

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, aah, sijaleta amendment kwa sababu, hata yaliyoletwa ni ya muhimu, lakini hoja yangu ni kwamba, kuna ya muhimu zaidi ambayo yalitakiwa yaletwe hayajaletwa. Kwa hiyo, wanapoleta walete yale ambayo Wabunge tunashauri na siyo yale wanayoyataka wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho japo umesema wameyaondoa, lakini kuna jambo lazima tujifunze hapa. Kuna changamoto kubwa ambayo nimeiona tangu Bunge lililopita, haya Mashirika ya Serikali haya yanapewa pesa, yanaenda kufanya vibaya, yanakufa. Yakifa wanaleta visheria hapa vya kubana zile sekta ambazo zilikuwa zinafanya cover up, zinasaidia kufunika yale mashimo ambayo sekta za Serikali au mashirika yameshindwa kufanya.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano. Hii Sheria ya Postal ililetwa inataka kuwazuwia watu wengine waliokuwa wanasafirisha vifurushi, wale wa mabasi na nini wasifanye kazi, lakini hawa posta walishindwa kufanya hiyo function na walipewa hela.

Mheshimiwa Spika, mimi nimekua naona Suzuki imeandikwa Postal Bank of Tanzania, Postal of Tanzania, zimekufa zote. Hakuna mtu aliyekuwa taken into task, hayo mashirika yamekufa, sasa hivi wanarudi wanasema ni marufuku mtu kusambaza atasambaza posta peke yake. ATCL is the Same business, TTCL the Same business…

SPIKA: Kengele ya pili imeshaita!

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)