Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Salome Wycliffe Makamba (7 total)

MHE. LUCY T. MAYENGA (K.n.y. MHE. SALOME W. MAKAMBA) aliuliza:-
Tatizo la kukatika umeme mara kwa mara katika Jimbo la Kahama Mjini linaathiri sana uzalishaji viwandani hasa ukizingatia Serikali imepiga marufuku kwa baadhi ya viwanda kama vile vya kukoboa mpunga na kusaga mahindi kutofanya kazi usiku:-
Je, Serikali ipo tayari kuruhusu viwanda Wilayani Kahama kufanya kazi masaa 24 ili kufidia uzalishaji unaokuwa haufanyiki kipindi umeme unapokuwa umekatika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Wycliffe Makamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa hakuna zuio lolote la Halmashauri ya Mji wa Kahama kwamba mashine za kukoboa mpunga na mahindi zisifanye kazi wakati wa usiku au saa 24. Changamoto iliyopo ni kwamba viwanda hivyo vinatumia umeme wa jenereta ambao hautoshelezi kuendesha mashine wakati wote, hivyo kumekuwa na tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara. Halmashauri imewasiliana na Meneja wa TANESCO Kahama na tayari tatizo hilo limeanza kushughulikiwa ili kupata umeme wa uhakika kutoka gridi ya Taifa ambapo tayari kituo cha usambazaji kimeanza kujengwa Kahama.
Mheshimiwa Spika, Halmashauri inahamasisha wawekezaji wa viwanda vidogo, vikiwemo vya kukoboa mpunga, mahindi na mazao mengine ili kupanua wigo wa mapato kupitia ushuru wa huduma (service levy) na ajira kwa vijana, hivyo hakuna sababu yoyote kwa Serikali kuzuia wawekezaji katika viwanda vidogo na vikubwa. Azma ya Serikali ni kupanua uwekezaji wa viwanda kadri iwezekanavyo kwa kuzingatia fursa zilizopo. Tunachofanya ni kuboresha mazingira yatakayosaidia uwekezaji huo ufanyike kwa faida, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha umeme wa uhakika unakuwepo.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI (K.n.y MHE. SALOME W. MAKAMBA) aliuliza:-
Wafanyakazi wa migodi ya uchimbaji wa madini hufukuzwa kazi kiholela bila kulipwa fidia stahiki kutokana na ulemavu na magonjwa yanayosababishwa na vitendea kazi hatarishi wakati wakiwa kazini.
(a) Je, Serikali iko tayari kuzuia kuingizwa nchini vitendea kazi hatarishi na kufunga migodi ambayo ina wahanga wengi na ulemavu na magonjwa yatokanayo na shughuli za uchimbaji madini?
(b) Je, ni lini Serikali itaanza kutumia Sheria ya Fidia Na. 20 ya mwaka 2008 ili wafanyakazi wa migodini walipwe fidia stahiki wanapopata ulemavu au magonjwa wanapokuwa kazini badala ya Sheria ya Fidia ya mwaka 2002? na
(c) Je, Serikali inatoa tamko gani kwa waajiri wanaowatelekeza wafanyakazi waliopata ulemavu wakiwa kazini na kukataa kuendelea kulipa gharama za matibabu yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri Mkuu naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Makamba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia taasisi zake na sheria mbalimbali za nchi inao utaratibu madhubuti wa kudhibiti uingizwaji wa bidhaa zisizo na ubora pamoja na vitendea kazi hatarishi kwa afya za wafanyakazi mahali pa kazi ikiwemo migodini.
Aidha, Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi ya mwaka 2003, imeipa mamlaka Wakala wa Afya na Usalama Mahali pa Kazi kukagua vitendea kazi vinavyotumika mahali pa kazi ikiwa ni pamoja na migodi na kupima afya za wafanyakazi.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi Namba 20 ya mwaka 2008 ilitungwa ili kulipa fidia kwa wafanyakazi wanaoumia au kupata madhara au kufariki wakiwa kazini, ikiwa ni pamoja na wafanyakazi wa migodini wanaopata ajali.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria namba 20 itaanza kutoa rasmi fidia kwa wafanyakazi tarehe 1/7/2016. Kipindi hiki waajiri wote waendelee kutumia Sheria Na. 263 kuhakikisha wafanyakazi wanahudumiwa na kulipwa wawapo kazini. Aidha, Serikali inatoa onyo kwa waajiri ambao hawataki kutenda haki ya kuwalipa fidia kwa mujibu wa sheria.
MHE. SALOME W. MAKAMBA aliuliza:-
Serikali kupitia Mawakala wake wa Maji katika Mkoa wa Shinyanga imepandisha bei ya maji kwa takribani asilimia 100 kwa unit na service charge.
Je, Serikali ina mpango gani wa kupunguza bei ya huduma ya maji ili wananchi waweze kumudu gharama za huduma hiyo na pia kuwavutia zaidi wawekezaji viwandani ili waendelee na uzalishaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Makamba, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Serikali kupitia Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira katika Manispaa ya Shinyanga (SHUWASA) imepandisha bei ya maji mwezi Septemba, 2015 kwa matumizi mbalimbali kwenye Manispaa hiyo.
Mamlaka hiyo ilipandisha bei hizo baada ya kupata kibali cha kufanya hivyo toka Mamlaka ya Udhibiti wa Maji na Nishati (EWURA). Bei hizo zimepandishwa kutoka shilingi 790 hadi shilingi 1,000 kwa ujazo wa lita 1,000 kwa matumizi ya majumbani ambayo ni sawa na asilimia 26 na shilingi 1,370 hadi shilingi 2,000 kwa ujazo wa lita 1,000 kwa matumizi ya viwandani ambayo ni sawa na asilimia 46.
Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kuongeza bei za maji ni wa kawaida na ni wa kisheria. Kabla ya kupandisha bei za maji mamlaka husika hulazimika kuomba kibali cha kufanya hivyo kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Maji na Nishati (EWURA) wakionesha sababu za kusudio la kupandisha bei hizo ambazo hujumuisha gharama za uendeshaji pamoja na sehemu ya uwekezaji wa miundombinu. EWURA kwa kuzingatia sheria, kanuni na ushirikishaji wa wataalam mbalimbali katika eneo au mji unaohudumiwa na mamlaka hiyo huendesha uchunguzi na mchakato wa kujiridhisha na uhalisia wa kupandisha bei hizo.
Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kupunguza bei za maji pale inapogundua gharama za umeme kwa ajili ya uzalishaji wa umeme utatumia gesi ya asili ambayo ina gharama nafuu kuliko ukizalisha kwa kutumia dizeli. Kwa maeneo ya vijijini gharama za uzalishaji zitapungua maeneo mengi kwani Serikali ina mpango wa kubadilisha mifumo ya mitambo ya maji kwa kutumia nishati ya jua.
MHE. SALOME W. MAKAMBA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Rais aliyoitoa wakati wa kampeni kwa wananchi wa Jimbo la Kahama Mjini ya kujenga kwa kiwango cha lami kilometa 10 za barabara za mitaa ya Mji wa Kahama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Wcyliffe Makamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya kwanza ya utekelezaji wa ahadi ya Mheshimiwa Rais ilikuwa ni kuzitambua barabara zitakazojengwa kwa kiwango cha lami katika Halmashauri ya Mji wa Kahama ambayo imekamilika. Ujenzi huo utahusisha barabara ya Mama Farida yenye urefu wa kilometa 1.305; barabara ya Phantom -Majengo yenye urefu wa kilometa 5.214; barabara ya Malunga Mashineni - Mwamvua yenye urefu wa kilometa 1.852, barabara ya Nyihogo - Namanga yenye urefu wa kilometa 0.6, barabara ya Florida - Stendi ndogo yenye urefu wa kilometa 0.829 na barabara ya Royal ya Zamani - Stendi Ndogo yenye urefu wa kilometa 0.2.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa barabara hizo utafanyika kwa awamu ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018, zimetengwa shilingi 603,604,733 kwa ajili ya kujenga barabara yenye urefu wa kilometa moja kwa kiwango cha lami. Vilevile, kupitia fedha za Mfuko wa Barabara, zimetengwa shilingi 320,000,000 kwa ajili ya ukarabati wa barabara za lami zenye urefu wa mita 800 katika Mji wa Kahama.
MHE. WILFRED M. LWAKATARE (K.n.y. MHE. SALOME W. MAKAMBA) aliuliza:-
Zaidi ya Kaya 800 za wananchi wa Mitaa ya Bukondamoyo na Muhunguala katika Kata ya Muhunguala, Jimbo la Kahama Mjini wamezuiliwa kupatiwa huduma muhimu za kijamii kwa madai kwamba wanaishi kando ya Bwawa la Nyihogo, ilihali wananchi hao wanaishi umbali wa zaidi ya mita 700 kutoka katika bwawa hilo:-
Je, ni kwa nini Serikali inawanyima wananchi hao huduma za kijamii wakati wako umbali wa mita 60 zilizowekwa kisheria?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Makamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Bwawa la Nyihongo ndiyo chanzo pekee mbadala cha maji katika Mji wa Kahama, ambapo bwawa hilo lilisanifiwa mwaka 1948, lenye eneo la zaidi ya ekari 145. Mipaka ya bwawa hilo ilitangazwa katika Gazeti la Serikali, Namba 72, mwaka 1963.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wengi wamevamia kwenye hifadhi ya eneo tengefu la bwawa hilo, hasa katika sehemu za kidakio cha maji na wengine wapo kwenye eneo hatarishi, linalopitisha maji baada ya bwawa kujaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Maji Kahama kwa kushirikiana na Uongozi wa Wilaya ya Kahama na Halmashauri ya Mji wa Kahama kwa ujumla umetoa ilani ya kusitisha shughuli zote za kibinadamu kufanyika ndani ya hifadhi ya bwawa na kidakio cha maji. Kutokana na hilo Serikali inaandaa mpango wa kuwaondoa wananchi hao katika maeneo hayo na kuendelea kuzuia shughuli za kibinadamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutoa huduma kwa kaya zote ambazo ziko nje ya mpaka wa hifadhi ya bwawa kwa kuwapatia huduma ya maji safi na inawashauri wananchi ambao wapo ndani ya hifadhi ya bwawa hilo kuhama ili kulinda chanzo hicho kwa manufaa yao wenyewe.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA (K.n.y. MHE. SALOME W. MAKAMBA) aliuliza:-

Je, kuna sababu gani za kitaalam zinazosababisha Walimu wa Shule za Sekondari kuhamishwa Shule za Msingi wakati ufaulu kwa Shule za Sekondari kwa masomo ya sanaa upo duni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Wycliffe Makamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilihamisha baadhi ya walimu waliokuwa wanafundisha shule za sekondari kwenda kufundisha shule za msingi katika mwaka wa fedha 2017/2018 ambapo walimu 8,693 walihamishwa. Walimu hao walihamishwa kutokakana na ziada ya Walimu wa masomo ya sanaa waliokuwepo katika shule za sekondari za Serikali nchini ambapo wakati huo shule za msingi za Serikali zilionekana kuwa na upungufu mkubwa wa Walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitaalam Walimu wote wa shule za msingi na sekondari wameandaliwa na wana mfanano katika maeneo ya mbinu za kufundisha, ya kisaikolojia na malezi na makuzi ya watoto wetu. Maeneo hayo ambayo kimsingi ni muhimu kwa kila Mwalimu na hufundishwa katika ngazi zote za vyuo vinavyotoa taaluma ya Ualimu nchini.

Naomba pia nilifahamishe Bunge lako Tukufu kuwa, suala la ufaulu duni husababishwa na sababu mbalimbali zikiwemo za kimazingira, ushiriki wa wazazi na jamii katika mchakato mzima wa ufundishaji na ujifunzaji kwa watoto. Hivyo, wingi wa Walimu pekee hautoshi kumfanya mwanafunzi afanye vizuri katika mtihani wake. Ahsante.
MHE. SALOME W. MAKAMBA aliuliza:-

Je, ni sifa zipi ambazo mzabuni anatakiwa kuwa nazo ili kupewa nafasi ya usimamizi mapato ya Serikali kwenye migodi midogo midogo (rush) kama Mwabomba, Namba Mbili, Segese na kadhalika?
WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Salome Wycliffe Makamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kutokana na juhudi kubwa zinazofanywa na Wizara katika kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo na kufungua masoko ya madini nchi nzima, kumesababisha ongezeko la wachimbaji wadogo ambao wamekuwa wakivamia maeneo mbalimbali (rush) kama vile kwenye maeneo yaliyotengwa, maeneo yenye leseni kubwa za utafiti, maeneo ya uchimbaji mkubwa, maeneo yasiokuwa na leseni na maeneo ambayo leseni zake hazijaendelezwa kwa shughuli za uchimbaji.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Tume ya Madini ilitoa Waraka wa Ndani Na. 3 ulioanza kutumika tarehe 15 Oktoba, 2019 wenye dhumuni la kutoa mwongozo kwa Maafisa Madini Wakazi na watumishi wengine katika kusimamia, kudhibiti shughuli za madini na mapato ya Serikali katika maeneo yenye rush. Kwa mujibu wa Waraka huo, utaratibu unaotumika kuwapata wasimamizi wa rush kama alivyouliza Mheshimiwa Mbunge, ni kupitia Kamati ya Uongozi inayofuatilia na kuimarisha usimamizi katika eneo la rush.

Mheshimiwa Spika, Kamati hiyo huteua wasimamizi wa rush ambapo Mwenyekiti wa rush anapaswa kuwa na sifa zifuatazo: Awe mchimbaji mzoefu hasa katika usimamizi wa maeneo ya aina hiyo; asiwe na historia ya wizi wa fedha za Serikali; na awe mwaminifu. Aidha, wajumbe wengine kwenye usimamizi wa rush ni pamoja na Katibu, Mweka Hazina, Mwenyekiti wa Kijiji, Mwenyekiti wa Kitongoji, Mjumbe wa REMA, TAWOMA na mwakilishi wa eneo/shamba.