Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Additional Questions to the Prime Minister from Hon. Lucia Ursula Michael Mlowe (1 total)

MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli sijaridhika kabisa na majibu ya Naibu Waziri, Jeshi la Zimamoto linafanya kazi katika mazingira magumu sana. Mfano, Mkoa wangu wa Njombe hawana ofisi, wanatumia majengo ya Idara ya Maji, hawana magari; na tukiangalia Mkoa wa Njombe kijiografia umekaa vibaya sana na matukio ya moto ni mengi.
Nilikuwa nataka kujua time frame, ni lini Serikali itatoa vifaa au vitendea kazi kwa Jeshi la Zimamoto?
Swali langu la pili, kwa kuwa huduma ya Zimamoto iko zaidi mijini, lakini matatizo ya moto yako mengi sana vijijini. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha hata watu wa vijijini wanapata huduma hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi kwamba tuna matatizo ya ofisi pamoja na vitendea kazi nchi nzima kwa Jeshi la Zimamoto; na ukiangalia katika Wilaya zote takribani za nchi nzima kwa upande wa Tanzania Bara ni Wilaya 20 ambapo kuna Ofisi za Zimamoto mpaka sasa hivi pamoja na magari.
Hata hivyo, Serikali imefanya jitihada kubwa sana kuhakikisha kwamba tunatanua wigo ili huduma hizo ziweze kufika mpaka vijijini na ndiyo maana tuna mpango sasa hivi wa kuhakikisha kwamba tunapeleka huduma za Zimamoto katika Wilaya zote nchini hatua kwa hatua kwa kuanza kupeleka Maofisa ili waweze kutoa elimu na baadaye kadri vifaa vitakavyopatikana tutapeleka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na magari pamoja na vitendea kazi, katika bajeti ya mwaka huu tumetenga takriban shilingi bilioni 1.5 kununua magari mawili, tutaangalia ni maeneo gani ya kipaumbele tuweze kupeleka.
Naomba nichukue fursa hii kumwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutashauriana na Makao Makuu Idara ya Zimamoto tuone uharaka wa kufanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna mpango mwingine, tunafanya mazungumzo sasa hivi na Austria pamoja na Belgium, Kampuni ya SOMAT ya Belgium ili kuweza kupata mkopo wa Euro bilioni tano pamoja na Euro milioni 1.9 ambazo zitasaidia kuweza kununua vifaa viweze kupunguza makali ya upungufu wa vifaa katika maeneo mbalimbali nchini mwetu.